Balozi wa Pakistani nchini Siraj Ahmad Khan (kushoto), Mkurugenzi
wa Biashara wa Vodacom Tanzania, Linda Riwa (katikati) na Afisa Mtendaji
Mkuu wa kampuni ya Digit, Abdul Rehman Mahmood (kulia) wakiwa kwenye
picha ya pamoja wakati wa uzinduzi wa simu maalum iitwayo Smart Kitochi+
kwa ajili ya watu wenye ulemavu wa kuona na kusikia huku ikiongeza
matumizi ya dijitali nchini, hafla hiyo ilifanyika jana jijini Dar es
Salaam.
Ili
kuimarisha ushirikishwaji na kuongeza matumizi ya huduma na bidhaa za
kidijitali nchini, kampuni ya teknolojia na mawasiliano ya Vodacom Tanzania PLC
imezindua simujanja ya kidijitali inayoitwa 'Smart Kitochi +' ambayo imeundwa ikiwa
na vipengele muhimu kwa ajili ya wateja wasiosikia na wasioona.
Akizungumza
katika hafla ya uzinduzi jijini Dar es Salaam leo, Mkurugenzi wa Biashara wa kampuni
hiyo, Bi. Linda Riwa, amesema kuwa uzinduzi huu ni sehemu ya juhudi endelevu za
kampuni hiyo za kukuza ushirikishwaji huku ikiunga mkono serikali katika azma
yake ya kuchochea matumizi ya bidhaa na huduma za kidigitali.
"Tunafurahia
mapinduzi haya ya kuleta bidhaa na huduma za kidigitali na za kibunifu kwa
wateja wetu wenye mahitaji mbalimbali kote nchini. Leo, tunazindua simu ya
kipekee ya kidijitali inayoitwa 'Smart Kitochi+' ambayo mbali na sifa kama kioo
kikubwa na cha kugusa, uwezo mkubwa wa kuhifadhi na betri inayodumu muda mrefu,
simu hii pia itawanufaisha wateja wetu wenye ulemavu wa kusikia na kuona,”
anasema Linda.
“Simu
hii inajumuisha teknolojia ya kugusa na sauti, ikiruhusu wateja wenye
changamoto hizi kupata huduma zetu bila kutegemea msaada wa mtu mwingine. Haya
ni mapinduzi muhimu katika sekta ya utoaji huduma za mawasiliano, ikizingatiwa
kuwa serikali inahimiza watoa huduma kuzingatia ushirikishwaji katika utoaji wa
huduma kwa wateja,” aliongeza Linda.
Uzinduzi
wa simu hii ni ingizo la kipekee sokoni ukilinganisha na matoleo mengine, ikiwa
na uwezo wa kuchochea ushirikishwaji katika matumizi ya huduma za mawasiliano
ya kidigitali. Pia ina ubora wa hali ya juu ikiwa na kioo kikubwa na cha kugusa
(2.8”), uwezo mkubwa wa kuhifadhi vitu kwenye 8GB na betri inayodumu muda mrefu
ya 3000mAh.
Toleo
hili jipya la 'Smart Kitochi+' ni sehemu ya juhudi za Vodacom kuwapeleka wateja
wake kwenye matumizi ya kidigitali, ikiwa ni pamoja na mtandao wa 4G, ambao
bado una watumiaji wachache ikilinganishwa na idadi ya watumiaji wa simu za
mkononi nchini Tanzania.
"Tunajivunia
kuwa mtandao unaoongoza nchini, tukitoa huduma za kidigitali za ubunifu kwa
zaidi ya wateja milioni 21. Kuwa na idadi kubwa ya wateja pekee haitoshi;
tunataka wateja wetu wanufaike na mapinduzi ya kidigitali yanayoendelea na
ubunifu mkubwa tunaoingiza kwenye bidhaa zetu. Kwa kuanzisha bidhaa za kisasa
kama 'Smart Kitochi+' tunaamini tutachochea wateja wengi zaidi kuhama kutoka
kwenye mfumo wa 2G na kuanza kufurahia huduma mbalimbali za kidigitali
zinazotolewa na mtandao wetu wa kasi wa 4G na 5G uliosambaa nchini na hatimaye
kuongeza matumizi ya simujanja ambayo kwa sasa ni asilimia 32," alifafanua
Bi. Linda.
Akizungumzia
simu hiyo mpya, Mwenyekiti wa Chama cha Viziwi Tanzania (TLB) Bw. Luis
Benedicto aliisifia simu hiyo akikiri kuwa itakuwa mkombozi kwa watu wenye
ulemavu wa kusikia na kuona.
"Tulikuwa
tumetengwa na kubanwa katika matumizi ya simu za mkononi, kwani nyingi hazikuwa
rafiki kwa watu wenye ulemavu wa kusikia na kuona. Kuzinduliwa kwa simu hii
kutatusaidia sio tu kufurahia huduma za mawasiliano kutoka Vodacom bali pia
kuimarisha mwingiliano wetu na wengine na kutumia simu hizi kwa manufaa ya
kijamii na kiuchumi," alielezea Bw. Benedicto.
Uzinduzi
huu unakuja baada ya hivi karibuni kampuni hiyo kuanzisha dawati maalum kwa ajili
ya kuhudumia wateja wasioona baada ya kuanzisha dawati kama hilo kwa ajili ya
wateja wenye ulemavu wa kusikia mwaka jana.
Juhudi
za kampuni hiyo katika kuzingatia na kuboresha maisha ya wateja wake ili kupunguza
au kufuta kabisa utofauti uliopo wa kidigitali kwa watu wenye ulemavu
zimeifanya iwe miongoni mwa watia saini wa miongozo ya GSMA kwa kuchochea ushirikishwaji
wa kidigitali kwa watu wenye ulemavu. Miongozo hiyo huweka misingi ya hatua za
kuchukua pamoja na kinachotakiwa kufanywa na mtoa huduma za simu za mkononi ili
kupunguza pengo katika upatikanaji wa huduma pamoja na matumizi ya huduma hizo.