.......
Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa, ya Bunge la Uganda imeipongeza Serikali ya Tanzania kwa uwekezaji mkubwa iliyofanya katika ujenzi wa Chuo Kikuu cha Dodoma, pamoja na kusifu Amani na Utulivu mkubwa uliopo, kwa kuzingatia idadi kubwa ya wanafunzi wanaosoma chuoni hapo.
Pongezi hizo zimetolewa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Gilbert Olanya, wa Jimbo la Kilak Kusini, Alhamisi tarehe 18 Aprili 2024, walipofanya ziara ya kutembelea maeneo mbalimbali ya chuo hicho pamoja na kufanya mazungumzo na Makamu Mkuu wa Chuo, Prof. Lughano Kusiluka, kwenye ofisi yake iliyopo jengo la Benjamin Mkapa, Dodoma.
Aidha, wamevutiwa na aina ya masomo yanayofundishwa katika Ndaki, Shule Kuu na Taasisi za Chuo, pamoja na namna chuo kinavyoendelea kuwekeza katika kuanzisha programu mpya za masomo zinazoakisi mabadiliko makubwa ya kisekta yanayozingatia utoaji mafunzo wenye kutatua changamoto kubwa za ajira, na matumizi ya teknolojia katika ufundishaji.
Akiukaribisha ujumbe huo, Makamu Mkuu wa Chuo, Prof. Kusiluka amelishukuru Bunge la Tanzania kwa kuona umuhimu wa kuwaleta wabunge hao kuja kujifunza UDOM, na kueleza ni kwa namna gani wabunge hao wana mchango mkubwa katika kuongeza hamasa ya ufundishaji wa lugha ya Kiswahili katika Nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki, na kutunga Sera zenye kusaidia nchi hizo kuendana na mabadiliko makubwa ya kisanyansi na teknolojia katika Sekta ya Elimu.
Aidha, amewahamasisha waganda kuja kusoma Tanzania kutokana na uwepo wa mitaala mizuri na masomo yenye kukidhi mahitaji katika soko la Afrika Mashariki na Afrika kwa ujumla.
“Tunayo fursa ya wananchi wa Uganda na nchi nyinginezo za Afrika Mashariki kuja kusoma UDOM. Niwahakikishie tunayo mazingira mazuri na thabiti ya kujifunzia kwa wana Afrika Mashariki kuja kusoma Tanzania. Mazingira yetu, tamaduni na mahitaji yetu yanafanana, kwangu mimi hii ni fursa kwetu sote” alisisitiza
Wajumbe wengine wa Kamati hiyo waliofika kutembelea Chuo Kikuu cha Dodoma ni pamoja na Mhe. Betty Ethel Naluyima, Mhe. Dkt. Isingoma Patrick Mwesigwa, Mhe. Rwemulikya Ibanda Gerald, Mhe. Patrick Ocan na Mhe. Lillian Obiale Paparu.
Wajumbe wa Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa, wa Bunge la Uganda, wakiwa kwenye mazungumzo na Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dodoma, Prof. Lughano Kusiluka, ofisini kwake Dodoma.
Wakiwa kwenye picha ya pamoja ni ujumbe kutoka Uganda, wakiwemo wabunge wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa, wa Bunge la Uganda. Katikati ni Mhe. Gilbert Olanya, wa Jimbo la Kilak Kusini, Mwenyekiti wa Kamati; na kushoto kwakwe ni Prof. Lughano Kusiluka, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dodoma, (aliyevaa Kaunda).
Prof. Lughano Kusiluka akikamkabidhi zawadi ya ukumbusho Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa, Uganda, Mhe. Gilbert Olanya. Wabunge hao walifika kutembelea chuo na kujifunza mambo mbalimbali yanayohusu utoaji wa Elimu ya Juu nchiniTanzania.
Viongozi wa Chuo Kikuu cha Dodoma wakiagana na waheshimiwa wabunge wa Uganda, baada ya kuhitimisha ziara yao chuoni hapo.
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameendelea kutenga fedha za kutekeleza miradi ya nishati ambapo katika kipindi cha miaka mitatu zaidi ya shilingi trilioni 8.18 zilitolewa.
“Maono na maelekezo yake kuhusu usimamizi wa sekta hii yamekuwa na mchango mkubwa katika ufanisi wa shughuli za sekta, katika hili, ninampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kuweka kipaumbele kikubwa katika utekelezaji wa miradi ya nishati.”
“Katika kuhakikisha upatikanaji wa uhakika wa umeme nchini, tayari nchi yetu imeanza kutumia umeme wa bwawa la Julius Nyerere Hydropower Project (JNHPP). Huu ni ushindi na kielelezo tosha kwamba Mama yupo kazini.”
Ametoa pongezi hizo leo jioni (Ijumaa, Aprili 19, 2024) wakati akifunga Maonesho ya Wiki ya Nishati yaliyofanyika kwenye viwanja vya Bunge jijini Dodoma.
Waziri Mkuu amelipongeza Shirika la Umeme Nchini (TANESCO) kwa kuweza kuzalisha umeme zaidi ya mahitaji yaliyopo sasa. “Leo tarehe 19 Aprili, 2024 uzalishaji wa umeme ni mkubwa. Shirika letu la TAMESCO limemudu kuzalisha umeme zaidi ya mahitaji tuliyonayo na bwawa la Julius Nyerere Hydropower Project limeanza kazi na tayari megawati 235 ziko kwenye mfumo.”
Ameitaka Wizara hiyo iweke mkakati wa kuhakikisha maonesho hayo yanakuwa endelevu ili Waheshimiwa Wabunge waweze kupata fursa ya kuwasilisha hoja zao mahsusi na kutatua kero za wananchi wanaowawakilisha.
Kutokana na kuongezeka kwa idadi ya washiriki wa maonesho hayo ikilinganishwa na miaka miwili iliyopita, Waziri Mkuu ameitaka Wizara hiyo ione uwezekano wa kuandaa maonesho kama hayo katika ngazi ya Mikoa na Halmashauri. “Wakurugenzi wa Kanda na Mameneja wa Mikoa na Wilaya mko hapa. Nendeni mkae na muangalie jinsi ya kutekeleza jambo hilo,” amesisitiza.
Ameitaka Wizara hiyo iweke mkakati wa kuhakikisha wananchi wote wanapata ufafanuzi wa masuala mbalimbali kuhusu fursa zinazopatikana kutokana na miradi inayotekelezwa na sekta ya nishati. “Pamoja na kuyaleta maonesho hapa Bungeni, kuna haja ya kupeleka maonesha kama haya kwenye maeneo ya katiati ya mji ili muweze kuwafikia wananchi wengi zaidi na kujibu hoja zao,” amesema.
Mapema, akimkaribisha Waziri Mkuu kuzungumza na wadau mbalimbali walioshiriki maonesho hayo, Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dkt. Doto Biteko ameipongeza TANESCO kwa kuendelea kufanya kazi nzuri ya kuhakikisha wananchi wanapata nishati ya umeme.
Naye, Spika wa Bunge la Tanzania, Dkt. Tulia Ackson amesema sekta ya nishati ni kati ya sekta mtambuka kwa sababu inalisha sekta nyingine nyingi na ikitikisika, inatikisa na maeneo mengine pia.
Amesema pamoja na utoshelevu wa umeme kwenye gridi ya Taifa, ili kuwe na maendeleo bado nchi inahitaji umeme wa kutosha na hasa kwenye viwanda na siyo kuwasha taa za majumbani.
Ameitaka Serikali itafute njia ya kutumia vizuri maji yanayotoka kwenye bwa la JNHPP ili yaweze kuwanufaisha wananchi wanaoishi maeneo ya jirani na bwawa hilo. “Bwawa limejaa kwa hiyo Serikali ihakikishe maeneo ya jirani yanapata maji ya kutumia. Tuanzishe gridi ya maji kama ilivyo kwenye gridi ya umeme. Kule chini tutengeneze njia ya kutunza maji kwa ajili ya matumizi ya umwagiliaji na mifugo,” amesema.
Naye, Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Mhandisi Felchesmi Mramba amesema ushiriki wa mwaka huu umevunja rekodi kwani watu zaidi ya 480 walitembelea maonesho hayo ambapo 267 walikuwa ni Waheshimiwa Wabunge.
Ameyataja maeneo ambayo washiriki walikuwa wakiulizia zaidi ni umeme, nishati ya jua, nishati jadidifu, nishati safi ya kupikia, mafuta na gesi.
Amesema ili kujenga uelewa mpana kwa wananchi, wanapanga kuandaa kongamano maalum juu ya gesi asilia ambalo linatarjiwa kufanyika Mei, mwaka huu.
-Apongeza Serikali Njombe mrejesho kwa wananchi, chama kwa usimamizi
Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dk Emmanuel John Nchimbi, amesema kazi kubwa iliyofanywa na Serikali, chini ya uongozi wa Rais Dk Samia Suluhu Hassan, ndani ya miaka mitatu, ni nyezo inayobeba ukweli wa kutosha kusambaratisha uongo unaoenezwa na baadhi ya wapinzani wa kisiasa kupitia mikusanyiko yao.
Amewataka wana-CCM wote kuendelea kujiamini na kutembea kifua mbele wanapozisema, kuzitangaza na kuikumbusha jamii kuhusu kazi za maendeleo na ustawi wa jamii, zinazofanywa na Serikali za CCM ili wananchi waendelee kuuona ukweli, wakitofautisha na uongo unaoenezwa kwa propaganda nyepesi za kisiasa.
Balozi Nchimbi amesema hayo leo, Aprili 19, 2024, alipokuwa akiwahutubia maelfu ya wanaCCM wa Mkoa wa Njombe, kupitia Mkutano Maalum wa Mkoa, uliofanyika mjini Njombe.
“Mambo yaliyofanywa na Serikali ndani ya hii miaka mitatu, unaweza kuona kama ni miujiza. Kazi kubwa sana inafanyika. Ni wajibu wetu kuitumia nyenzo yenye ukweli kupambana,” amesema.
Kupitia mkutano huo, ambao Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Antony Mtaka aliwasilisha taarifa ya mrejesho wa utekelezaji wa Ilani ya CCM ya 2020 - 2025, iliyohusisha miradi mbalimbali ya maendeleo na ustawi wa wananchi, Balozi Nchimbi pia amerudia kusisitiza kwa watendaji wa Chama na Serikali ulazima na umuhimu wa kuwa waadilifu wakati wote kwenye masuala yanayohusu rasilimali za umma, kwa kupiga vita rushwa na ubadhirifu.
Dk Nchimbi, akiambatana na Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa (NEC), Oganaizesheni, Ndugu Issa Haji Usi Gavu na Katibu wa NEC, Itikadi, Uenezi na Mafunzo, Ndugu Amos Gabriel Makala, yuko mkoani Njombe kwa ziara ya siku mbili, ikiwa ni mwendelezo wa ziara yake katika mikoa 6 ya Katavi, Rukwa, Songwe, Mbeya, Njombe na Ruvuma.
Amesisitiza kwamba pamoja na ugumu wa kukarabati bwawa hilo wakati likiwa na maji maamuzi magumu yafanyike wataalamu wa Wizara ya Maji watumie utaalamu wao kulifanikisha hiko kwani hakuna namna nyingine.
Akizungumza na mamia wa wananchi wa Kata za Lepruko, Sepeko, na Makuyuni Waziri wa maji maelekezo kwa Wataalamu wa Wizara kama ifuatavyo kwanza kutumia taaluma zao kuhakikisha Bwawa hilo linakarabatiwa kwa dharula haraka kuanzia kesho tarehe 19.04.2024 kudhibiti maji kuebdelea kupotea pili kufanya usanifu wa kina nyakati za kiangazi kusudi bwawa hilo liweze kukarabatiwa kwa uhakika zaidi.
Katika hatua nyingine Mbunge wa Jimbo la Monduli Mh Fred Lowassa amesema Bwawa hilo ndio tegemeo la wana Monduli kwenye matumizi ya maji kwa Binadamu, mifugo na wanyamapori hivyo anaiomba Serikali ione namna ya kukarabati bwawa hilo kwa dharura.
Aidha, Wakizungumza katika nyakati tofauti madiwani wa kata zinazoguswa na bwawa hilo wameishukuru serikali inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt Samia Suluhu Hassan kuwafikia kwa haraka na kutafuta suluhu ya utatuzi ya changamoto hii.
WAZIRI wa Ardhi,Nyumba na Mendeleo ya Makazi Jerry Silaa anatarajiwa kuongoza Kliniki ya Ardhi kwa mkoa wa Tanga itakayofanyika kuanzia Aprili 22 mpaka 28 mwaka huu ikifanyika kwenye maeneo mawili Kijiji cha Miaka 21 Chumbageni Tanga na Korogwe.
Akizungumza na waandishi wa habari leo,Kamishna Msaidizi wa Ardhi mkoa wa Tanga Tumaini Gwakisa alisema zoezi hilo litafanyika kwenye maeneo mawili ambapo litaanzia Ofisi ya Kamishna wa Ardhi Msaidizi wa Mkoa wa Tanga eneo la Kijiji cha miaka 21 Chumbageni kuanzia Aprili 22 mpaka 25 mwaka huu.
Alisema baada ya kumaliza kwa Tanga wataelekea wilayani Korogwe ambapo litafanyika kuanzia Aprili 26 mpaka 28 mwaka hu na uendeshwaji wa program hiyo utasimaiwa na itaongozwa na Waziri wa Ardhi Jerry Silaa akiwa na wataalamu wa Wizara hiyo.
“Nichukue nafasi hii kwaalika wananchi wote wa mkoa wa Tanga kuhudhuria na kupata huduma mbalimbali za sekta ya ardhi katika maeneo ambayo kliniki hiyo itafanyika kwani kutakuwa na utatuzi wa migogoro ya ardhi ambapo Waziri atasikiliza kero mbalimbali za Migogoro hiyo”Alisema
Alisema pia kutakuwa na utolewaji wa elimu kuhusu usimamizi wa ardhi pamoja na uwepo wa kituo jumuishi kitakachotoa huduma ya kupokea maoni mbalimbali na utoaji hati miliki ,ukadiriaji wa kodi ya ardhi na ulipaji wa kodi ya ardhi.
Gwakisa aliwataka wananchi wa mkoa wa Tanga kuhudhuria na kushiriki ambapo Waziri atakuwepo na wataalamu kutoka Wizarani
Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Mhe. Patrobas Katambi amesema Serikali ya awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuyapa kipaumbele masuala ya maendeleo ya vijana nchini.
Aidha, Mhe. Katambi amesema vijana ni nguvu kazi ya taifa, hivyo kuwezesha kundi hilo kunatoa fursa kubwa ya kuongeza kasi ya ukuaji wa uchumi na kuwafanya vijana kuwa chachu kwa maendeleo ya nchi.
Ameyasema hayo wakati wa hafla ya uzinduzi wa Programu ya Mpango wa Ulinzi wa Vijana Awamu ya Pili “Safeguard Young People (SYP)” iliyofanyika jijini Dar es Salaam.
Vile vile, Naibu Waziri Katambi amesema serikali imeboresha mwongozo wa utoaji mikopo kupitia mfuko wa maendeleo ya vijana ambapo kwa sasa mfuko huo unatoa mikopo kwa kijana mmoja mmoja, ambapo maboresho hayo yatawawezesha vijana walio katika sekta isiyo rasmi na wahitimu wa vyuo kujiajiri kwa kuanzisha miradi ya uzalishaji mali.
Kwa upande wengine, Mhe. Katambi amesema programu ya Safeguard Young People ni fursa kwa vijana kujikwamua na changamoto za kijamii na kiuchumi, hivyo amehamasisha ushirikiano katika utekelezaji wa programu hiyo ili kufikia malengo na kuleta mabadiliko chanya kwa vijana.
Naye, Balozi wa Switzerland Nchini Tanzania, Mhe. Didier Chassot amesema ni wakati wa kutambua mchango wa vijana katika kukuza maendeleo ya taifa. Aidha, ameongeza kuwa serikali ya Uswisi itaendelea kushirikiana na Tanzania katika kutekeleza programu hiyo ya SYP kwa lengo la kuwaondolea vijana changamoto za kiafya, kiuchumi, kisaikolojia na kijamii.
Akizungumza mmoja wa wanufaika amesema programu hiyo imewasaidia vijana kujitambu, kijithamini na kuwa na uthubutu katika kufanya maamuzi sahihi.
Programu ya Mpango wa Ulinzi wa Vijana “Safeguard Young People (SYP)” inalenga kuboresha huduma za afya, elimu ya afya kwa vijana, kuongeza ushirikishwaji wa vijana katika ngazi za maamuzi na pia kuwaunganisha vijana na fursa za kujipatia ujuzi na kipato.
Wasanii wa muziki wa kizazikipya Ben Pol, Phina na Tommy Flavor wakitoa burudani wakati wa hafla hiyo ya uzinduzi wa Programu ya Mpango wa Ulinzi wa Vijana Awamu ya Pili “Safeguard Young People (SYP II), iliyofanyika jijini Dar es Salaam.
Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Mhe. Patrobas Katambi (kushoto) akiteta jambo na Mwakilishi Mkazi wa UNFPA Tanzania, Mark Shreiner (kulia). Katikati ni Balozi wa Switzerland Nchini Tanzania, Mhe. Didier Chassot.
PICHA NA OFISI YA WAZIRI MKUU
(KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU)
NA EMMANUEL MBATILO, MICHUZI TV
KAMPUNI ya Oryx Gas na Taasisi ya Doris Mollel Foundation wamekabidhi mitungi ya gesi ya kupikia ya Oryx 50 kwa wauguzi katika Hospitali ya Rufaa ya Mwananyamala jijini Dar es Salaam kati ya mitungi 1000 inayotarajiwa kukabidhiwa kwa wauguzi na madaktari katika mikoa 10 nchini .
Akizungumza wakati wakisaini makubaliano ya ushirikiano yaliyofanyika katika hospitali ya rufaa ya Mwananyama, Mkurugenzi wa Kampuni ya gesi ya oryx Araman Benoite amesema makubaliano walioingia baina ys kampuni hiyo na taasisi ya Doris Mollel ni kusaidia kuongeza matumizi ya nishati safi ya kupikia kwa watanzania.
Aidha amesema katika kampeni hiyo ya kuwezesha watanzania kuingia katika matumizi ya nishati safi ya kupikia, mpaka sasa tayari wameshatoa mitungi kwa wananchi zaidi ya elfu 32 ili kusaidia lengo la kufikia asilimia 80 ya watumiaji wa nishati safi.
Amesema matumizi ya nishati safi ya kupikia inasaidia kuondoa hatari za kiafya kwa watumiaji wa kuni na mkaa kama nishati ya kupikia lakini pia hatari za kimazingira na ustawi wa jamii.
"Takribani watu 33,000 wanapoteza maisha nchini Tanzania kwa maradhi yanayotokana na kuvuta moshi unaotokana na mkaa au kuni hiyo ndio sababu ya Oryx gas kuja na suluhisho la kuwahamasisha wananchi kutumia gesi kwa matumizi ya kupikia", amesema Benoite
Ameeleza kuwa matumizi ya gesi yanaepusha wamama na watoto kuumika kubeba kuni hivyo kuepuka kujeuriwa na wanyama wakali wakiwa katika harakati za kutafuta kuni pia kuimarisha maisha ya wanawake na kuwalinda dhidi ya vitendo vya udhalilishaji.
“Kuanzia mwezi wa saba mwaka 2021 tumekuwa mstari wa mbele kuunga mkono utekelezaji wa mkakati wa serikali uliopewa nguvu na Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania , Dk. Samia Suluhu Hassan kwa lengo kwamba ifikapo mwaka 2033 asilimia 80 ya Watanzania wawe wanatumia nishati safi ya kupikia”, ameeleza.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Taasisi ya Doris Mollel , Doris Mollel amesema katika makubaliano waliosaini na oryxy watawafikia waguzi elfu moja ambapo watawapa mitungi na majiko ya gesi kama mabalozi kwa kina mama waweze kutumia nishati safi ya kupikia ikiwa ni programu ya miaka miwili.
Amesema mitungi hiyo itakwenda kwa wauguzi walioko maeneo magumu ambapo watakuwa wanawatembelea kwenye vituo vya afya na zahanati ili kuweza kuwafikia wafanyakazi ambao ni wauguzi wanaofanya kazi kubwa ya kuokoa maisha hususani ya mama na mtoto.
Wakati huo huo Mganga Mfawidhi Hospitali ya Rufaa ya Mwananyamala Dk.Zavery Benela ameeleza kwamba hospitali hiyo inakabiliwa na ongezeko la wagonjwa wa mifumo ya hewa.
Amefafanua kati ya wagonjwa wa nje 500 wanaofika kuonwa na madaktari bingwa asilimia 30 ya wagonjwa hao ni wa matatizo ya mfumo wa hali ya hewa unaosababishwa na hali ya hewa pamoja na mazingira ya kuandaa chakula kutokna na kuni na mkaa.
Aidha Dokta Benela amesema magonjwa ya mfumo wa hali wa hewa yamekuwa changamoto hasa kwa watu wazima na watoto.
Mkurugenzi wa Taasisi ya Doris Mollel , Doris Mollel (katikati) akizungumza katika hafla ya utiaji saini ya makubalinao na Kampuni ya Oryx Gas kushirikiana kuwezesha nishati safi ya kupikia kwa wauguzi na madaktari 1000 kutoka mikoa 10 nchini watakabidhi mitungi ya kupikia ya Oryx Gas lengo likiwa kuliwezesha kundi hilo la sekta ya afya kuondokana na matumizi ya kuni na mkaa. Hafla hiyo imefanyika leo Aprili 19, 2024.
Baadhi ya wauguzi wa hospitali ya rufaa ya Mwananyamala wakifuatilia hafla ya utiaji saini kati ya kampuni ya Oryx Gas na Taasisi ya Doris Mollel Foundation kuwezesha nishati safi ya kupikia kwa wauguzi na madaktari 1000 kutoka mikoa 10 nchini watakabidhi mitungi ya kupikia ya Oryx Gas lengo likiwa kuliwezesha kundi hilo la sekta ya afya kuondokana na matumizi ya kuni na mkaa. Hafla hiyo imefanyika leo Aprili 19, 2024.