Na Mwandishi wetu- Dodoma

Serikali kupitia Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu inaendelea kuratibu utekelezaji wa Mpango wa Taifa wa Dharura wa Kuzuia na Kukabiliana na Madhara ya El Nino kuanzia Septemba 2023 hadi Juni 2024.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Idara ya Menejimenti ya Maafa-Ofisi ya Waziri Mkuu (SBU) Brigedia Hosea Ndagala katika Kikao Kazi cha kujadili utekelezaji wa Mpango wa Taifa wa Dharura wa Kuzuia na Kukabiliana na Madhara ya El Nino Septemba 2023 hadi Juni 2024 ambapo alisema kutokea kwa maafa husababisha madhara ambayo huathiri utendaji kazi, kuzorotesha maendeleo na ukuaji wa kiuchumi kwa wananchi na kupotea kwa mafanikio yaliyopatikana kwa muda mrefu na hivyo, kuzorotesha hatua za maendeleo.

Alisema Maafa hayo yamekuwa yakisabibisha madhara mbalimbali ikiwemo vifo, ulemavu wa kudumu, upotevu na uharibifu wa mali na miundombinu, na ongezeko la tegemezi kutokana na Watoto kupoteza wazazi.

“Nchi yetu imekuwa ikishuhudia matukio ya majanga ambayo yamekuwa yakisababisha maafa na kuathiri mfumo wa kawaida wa maisha ya jamii. Maafa haya yamekuwa yakisabibisha madhara mbalimbali ikiwemo vifo, ulemavu wa kudumu, upotevu na uharibifu wa mali na miundombinu,”Alisema Brigedia huyo.

Aidha Brigedia Ndagala alizitaka kila sekta kuwasilisha tathmini ya utekelezaji wa Mpango wa Taifa wa Dharura wa Kuzuia na Kukabiliana na Madhara ya El Nino ambao una lengo la kuhakikisha serikali na wadau wanachukua hatua stahiki kuzuia au kupunguza madhara na kujiandaa kukabili na kurejesha hali kutokana na maafa yanayosababishwa na El Nino ili kuokoa maisha na mali.

“Hatua hii ni muhimu ili kuweka mikakati ya pamoja kwa ajili ya maandalizi ya msimu wa mvua za Masika. Ni imani yangu kuwa kikao kazi hiki kitatoka na mikakati madhubuti itakayosaidia kuendelea kuongeza ufanisi katika kukabiliana na maafa,” Alieleza.
 

Mkurugenzi Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Brigedi Hosea Ndagala akizungumza wakati akifungua Kikao Kazi Cha Kujadili Utekelezaji Wa Mpango Wa Taifa Wa Dharura wa Kuzuia na Kukabiliana na madhara ya mvua za El Nino kikao kilichofanyika Jijini Dodoma.
 

Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Luteni Kanali Selestine Masalamado akichangia wakati wa wasilisho la Madhara yaliyotokana na mvua za El-Nino katika kikao kazi kilichofanyika Jijini Dodoma.
 

Mkurugenzi wa Udhibiti na Usimamizi wa Ubora wa huduma za hali ya hewa kutoka Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) Bw. Geofrid Chikojo akitoa wasilisho kuhusu taarifa ya muelekeo wa mvua za msimu wa masika kwa mwezi Machi hadi Mei 2024 katika kikao kazi kilichofanyika Jijini Dodoma.
 

Katibu Tawala Msaidizi Mipango na Uratibu Mkoa wa Morogoro Ndug. Anza-Amen Ndossa akichangia mada wakati wa wasilisho lililohusu madhara yaliyotokana na mvua za El-Nino katika kikao kazi kilichofanyika Jijini Dodoma .
 

Picha ya pamoja ya washiriki wa kikao kazi cha Kujadili Utekelezaji Wa Mpango Wa Taifa Wa Dharura wa Kuzuia na Kukabiliana na madhara ya mvua za El Nino katika kikao kazi kilichofanyika Jijini Dodoma.

 

Na Mwamvua Mwinyi, Pwani Machi 29

Mufti wa Tanzania, Sheikh Abubakar Zubeir, anatarajia kuzindua rasmi kitabu chake ambacho kinahusu masuala mazima ya maadili, kitabia ndani ya jamii hususan kwa kundi la vijana, ifikapo mfungo mosi.

Aidha amewaasa watanzania kujenga tabia ya kusaidia makundi maalum pamoja na watoto wanaoishi kwenye mazingira magumu (yatima) kwa nyakati zote isiishie mwezi mtukufu wa Ramadan pekee.

Sheikh Zubeir alisema hayo katika iftari iliyoandaliwa na Rais dkt Samia Suluhu Hassan na kusimamiwa na Serikali mkoa wa Pwani, ambapo watu 500 wakiwemo watoto wanaoishi kwenye mazingira magumu 300 ,wazazi wao , viongozi mbalimbali wa vyama vya siasa , Taasisi na waalikwa wengine walijumuika katika futari hiyo.

Alieleza ,suala la maadili ni pana hivyo ni lazima kushirikiana ili kuwa na kizazi chenye maadili mema.

Sheikh Zubeir alitoa rai kwa jamii hususan kundi la vijana kutengeneza misimamo katika maadili na tabia njema ,ili kuwa na Taifa lenye maadili na mfano wa kuigwa Duniani.

"Ili Taifa lisimame vizuri na kuwa Taifa bora lazima kuwa na maadili kwani Hakuna Taifa bora ambalo linasimama pasipo watu wake kuwa na maadili bora" alisisitiza.

Vilevile alieleza kitendo cha Mkuu wa Mkoa wa Pwani Alhaj Abubakar Kunenge kufuturisha futari kwa kula pamoja na watoto wanaoishi kwenye mazingira magumu ni jambo jema lakuigwa.

"Watoto hawa wanahitaji faraja ,wasiojiweza wasaidie na isiwe mwezi mtukufu wa Ramadan hata nyakati nyingine ,na tukijenga tabia hii ya kusaidia tutajikuta tunafikia kundi kubwa" aliongeza Sheikh Zubeir.

Awali Mkuu wa Mkoa wa Pwani Alhaj Abubakar Kunenge alieleza, mwaka 2023 alitoa futari Mkoani Pwani, Machi 27  Dodoma na Machi 28 mwaka huu mkoa umesimamia watu 500 Kati yao watoto wanaoishi kwenye mazingira magumu 300 wamejumuika kufuturu .

Kunenge alimshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa kujali makundi maalum.

Mkuu huyo wa mkoa, aliziasa Taasisi zinazojihusisha kulea watoto ambazo zinakwenda kinyume na mikataba kwa kujinufaisha matumbo yao waache mara moja ,na wanachotakiwa ni kutekeleza malengo yao kwa watoto hao.

Nae Sheikh wa Mkoa wa Pwani, Khamis Mtupa
alisema waumini wa kiislam waendeleze kufanya yaliyo mema katika kipindi hiki cha mwezi mtukufu wa Ramadan.

Alieleza,kutoa ni imani Hata kama ni kidogo na kwa kutambua hilo Wana kamati maalum ambayo wanafikia wasiojiweza, gerezani ,mashuleni ili nao waweze kupata futari.

Mtupa aliomba watanzania kuendelea kuliombea Taifa Amani na kumuombea Rais dkt Samia kufanya majukumu yake kwa afya bora.






 

 

Dar es Salaam Ijumaa 29 Marchi 2024 BancABC Tanzania, ambayo ni kampuni tanzu ya Atlas Mara imetoa msaada wa vyakula mbali mbali pamoja na kuandaa futari kwa watoto wanaolelewa kwenye kituo cha watoto yatima cha New Faraja kilicho Mburahati Jijini Dar es Salaam ikiwa ni ishara ya kuonyesha upendo kwenye kipindi hiki cha Mwezi Mtukufu wa Ramadan.

Akizungumza Jijini Dar es Salaam mara ya kukabidhi msaada huo, Mkuu wa Idara ya Udhibiti BancABC Tanzania Saleh Geva alisema benki hiyo imetoa msaada pamoja na kufuturisha kituo cha Watoto yatima cha New Faraja kama ishara ya kuonyesha upendo pamoja na kuwapa tabasamu na hasa kwenye kipindi hiki cha Mwezi Mtukufu wa Ramadan. 

‘Watoto wanaoishi kwenye mazingira magumu wanahitaji kuonyesha upendo. Sisi BancABC Tanzania na hasa wafanyakazi tumefarajika sana kujumuika nao pamoja na kupata wasaa wa kufuturu na watoto wanaolelewa kwenye kituo hiki. Kilikuwa ni kipindi faraja sana kwao lakini furaha kwetu kuona watoto hawa wakitabasamu. Lengo letu ilikuwa ni kufanikiwa kuona watoto hawa wajisikia kama sehemu ya Jamii ya Watanzania’, alisema Geva.

Geva aliongeza ‘Kuwafanya watoto hawa watabasamu na kufurai kunawapa matumaini yao ya maisha ya baadae. Kuja kwetu kufuturu na watoto hawa kumetuonyesha kwa nini BancABC Tanzania imekuwa ikijikita sana kwenye kusaidia Jamii ambayo inayotuzunguka. Tutaendelea na utamanduni huu wa kusaidia Jamii ambayo inaishi kwenye mazingira mangumu kwa sababu tunaamini ni moja Kati ya nguzo ya sisi kuendelea kukua kibiashara’,

‘Furaha yetu sisi BancABC Tanzania ni kuona tukibadilisha maisha ya Watanzania. Tunaamini kwenye Jamii yenye usawa na ndio sababu mwaka huu tuliamua kuja kufuturu na watoto hawa ambao wanaishi kwenye mazingira magumu ’, alisema Geva.

‘BancABC Tanzania, ikiwa ni taasisi ya kutoa huduma za kifedha imekuwa ikifanya kazi kubwa sana kuwafikia Watanzania na hasa wale ambao bado hawafikiwa na huduma za kibenki. Kwa sasa, BancABC Tanzania tunao mawakala zaidi ya 700 nchini kote’, alisema Geva huku akiongeza kuwa benki hiyo inayo akaunti maalum kwa ajili ya wajasiriamali wadogo na wa kati kwa ajili ya kutoa mikopo ya kuimarisha biashara zao’.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa kituo cha New Faraja Zamda Idrisa alisema kuwa wamefarijika kwa kuona taasisi binafsi kama BancABC Tanzania ikiunga mkono Jamii ambayo inaishi kwenye mazingira mangumu.

Aliongeza ‘Msaada wenu umekuja kwenye muda muafaka kwani watoto hawa wanahitaji kuonyesha upendo kama watoto wengine. Tunawashukuru kwa msaada wenu na tunawaombea kwa Mwenyezi Mungu azidi kuwafungulia riziki kwenye maisha yenu ya kila siku’.

‘Tunatoa rai kwa taasisi zingine pamoja na watu binafsi wazidi kutusaidia kwani watoto hawa wanahitaji kuvaa, kusoma, chakula pamoja na matibabu na kituo chetu hakina wadhamini bali tunatengemea misaada kutoka kwa wadau mbali mbali kama BancABC Tanzania walivyokuja hapa kutusaidia kwa siku ya leo.


Mkuu wa Kitengo cha Idara ya Udhibiti BancABC Tanzania Saleh Geva akiwahudumia futari watoto wanaolelewa kwenye Kituo cha Watoto yatima cha New Faraja kilichopo Mburahati Jijini Dar es Salaam. BancABC Tanzania ambayo ni kampuni tanzu ya Atlas Mara ilitoa msaada wa vyakula mbalimbali pamoja na kuandaa futari kwa watoto waliopo kwenye kituo hicho kama ishara ya kuonyesha upendo kwenye kipindi hiki cha Mwezi Mtukufu wa Ramadan.
Baadhi ya watoto wanaolelewa kwenye kituo cha watoto yatima cha New Faraja kilichopo Mburahati Jijini Dar es Salaam wakifuatilia hotuba pamoja na nasaha kutoka kwa viongozi wa BancABC Tanzania mara baada ya benki hiyo kutoa msaada wa vyakula mbali mbali pamoja na kuwaandalia futari watoto hao ikiwa ni ishara ya kuonyesha upendo kwenye kipindi hiki cha Mwezi Mtukufu wa Ramadan.


Mkuu wa kitengo cha Udhibiti wa BancABC Tanzania (kulia) akimkabidhi msaada wa vyakula mbali mbali Mkurugenzi wa Kituo cha Watoto yatima cha New Faraja kilichopo Mburahati Jijini Dar es Salaam. BancABC Tanzania ambayo ni kampuni tanzu ya Atlas Mara ilitoa msaada wa vyakula mbalimbali pamoja na kuandaa futari kwa watoto waliopo kwenye kituo hicho kama ishara ya kuonyesha upendo kwenye kipindi hiki cha Mwezi Mtukufu wa Ramadan.

Na. Damian Kunambi, Njombe

Mkuu wa Wilaya ya Ludewa Victoria Mwanziva akiambatana na Mkurugenzi wa Halamashauri, viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) pamoja na wananchi wilayani humo wamefanya Dua/Kisomo Maalum cha kumuombea Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan ili azidi kupata kheri, hekmana baraka.

Akizungumza mara baada ya kufanyika kisomo hicho katika msikiti wa Wilaya ya Ludewa mkuu huyo wa wilaya amesema Rais Dkt. Samia amekuwa ni kiongozi anaye liongoza vyema Taifa la Tanzania hivyo anapopata baraka taifa zima linapata baraka pia kupitia yeye.

"Rais wetu amekuwa ni kiongozi bora na mwenye hekma, hivyo hatuna budi kumwombea kwa Mungu ili aweze kuendeleza ubora alio nao na kile ambacho Mungu amekiweka ndani yake".

Naye Mkurugenzi wa halmashauri ya Wilaya hiyo Sunday Deogratius amempongeza mkuu huyo wa Wilaya kwa kuandaa kisomo hicho kilicho ambatana na futari na kuongeza kuwa Rais Dkt. Samia amefanya maendeleo makubwa katika halmashauri mbalimbali ikiwemo halmashauri ya Wilaya ya Ludewa ambayo imepiga hatua kwenye maendeleo ya elimu, afya, miundombinu ya barabara na sekta nyinginezo.

Aidha kwa upande wake shekhe wa Wilaya hiyo Haruna Rahim amemshukuru mkuu wa wilaya kwa kuwaunganisha katika kufanya kisomo hicho pamoja na kupata futari kwani kwa kufanya hivyo kunaongeza Swawabu kutoka kwa mwenyezi Mungu na hasa katika kipindi hiki cha mfungo wa Ramadhan.

Kisomo hicho cha kumwombea Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kiliambatana na Iftari iliyo andaliwa na mkuu huyo wa Wilaya Victoria Mwanziva katika ukumbi wa Halmashauri ya wilaya hiyo ambapo waumini wote wa kiislamu na wageni waalikwa walijuika pamoja kupata ftari hiyo.

Sanjari na kisomo hicho na futari lakini pia mkuu huyo wa Wilaya alimkabidhi Shekhe Haruna zawadi ya pikipiki aina ya King lion 150 yenye thamani ya shilingi 2,600,000 milion ili iweze kumsaidia katika mizunguko yake mbalimbali huku mbunge wa jimbo la Ludewa akitoa hundi ya shilingi 1,000,000 kwaajili ya ujenzi wa msikiti.








Na Janeth Raphael -MichuziTv Dodoma

Naibu Waziri wa Afya Dkt. Godwin Mollel amewataka waganga wafawidhi nchini na Watumishi ndani ya Sekta ya Afya kutokuwa kikwazo kwa wawekezaji wanaotaka kuwekeza katika sekta hiyo ikiwemo uanzishaji wa vituo binafsi vya kutolea huduma za afya.

Pia amesema sekta binafsi imesaidia kwa kiwango kikubwa kuipunguzia Serikali mzigo hasa upande wa ajira kwani vijana wengi wameajiriwa kupitia sekta binafsi, hali ambayo sio rahisi kuiachia mzigo serikali pekee.

Dtk. Mollel ameyasema hayo Machi 27,2024 wakati akifunga Mkutano wa Kwanza wa Kimataifa wa Afya ya Msingi uliofanyika Jijini Dodoma kwa muda wa siku Tatu ambapo washiriki kutoka ndani na nje ya nchi wameshiriki na kuchangia mada zilizowasilishwa wakati wa mkutano huo.

Dkt. Mollel amewaasa Wakurugenzi wa OR- TAMISEMI na Wizara ya Afya kuangalia idadi ya Vijiji ambavyo havina Zahanati ili kuhakikisha vinapata vituo hivyo mapema iwezekanavyo.

“Tukijipanga kwa muda wa miaka miwili tukapunguza semina na makongamano na tukapunguza mambo mengine, tukapunguza kidogo kuboresha huku juu zaidi kwasababu huku tunaweza kwenda kwa pamoja, nawahakikishia kwa kipindi cha miaka miwili hakuna Kijiji kitakosa Zahanati”, amesema Mollel na kuongeza .

“Tunataka tutakapokutana tena katika mkutano wa mwaka 2026 tutazungumza masula mengine kama kuajiri watumishi, kuweka vifaa na kuboresha huduma zingine zinazopaswa kuongezwa” amesisitiza Mollel.

Aidha amewaomba washiriki katika mkutano huo kuwasaidia wakurugenzi ambao bado wanaleta mgawanyiko katika kazi kuhakikisha suala hilo wanalimaliza na kuimarisha utendaji zaidi.

“Sekta ya Afya ni moja na kazi nyingi za afya zinaanzia katika ngazi ya msingi na dada yangu Dkt. Grace amesisitiza hapa hakuna huduma za afya bila msingi kwani huduma zote zinaanzia huko kwa wananchi walio wengi ndipo wanaanzia kabla ya kuja huku juu kupatiwa huduma,” amesema.

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Afya Dkt.Grace Magembe amesema, ili kufanikiwa katika sekta ya Afya ni lazima kuboresha sekta kuanzia ngazi ya msingi na ustawi wa Jamii

"Hakuna Afya, bila kuhakikisha tunaboresha eneo la Afya ya Msingi na ustawi wa Jamii lipo sawa, mafaniko yetu tutaweza kujipima vizuri endapo tutatoa kipaumbele katika eneo la afya ya msingi," ameeleza Dkt. Magembe

Akitoa salaam za Ofisi ya Rais TAMISEMI, Katibu Mkuu Ofisi ya Rais TAMISEMI anayeshughulikia Afya Dkt. Charles Mahela, amesema kuwa kupitia mkutano huo mapendekezo kadhaa yameweza kutolewa kupitia majadiliano yaliyofanyika ikiwemo kuhakikisha upatikanaji wa fedha za kutosha kwa huduma za afya ya msingi.

“Mapendekezo hayo ni pamoja na kuongeza bajeti za afya za mifumo ya bima na jambo hili limesisitizwa kwa ukubwa na wakashauri vyanzo mbalimbali viweze kutumika ikiwemo kuwashirikisha wadau kama Wizara ya Fedha,”amesema.

Amesema pendekezo lingine lililotolewa ni kwa wadau pamoja na Serikali kuendelea kuwekeza katika miundombinu ya afya ya msingi, rasilimali watu na vifaa ili kuendelea kuboresha upatikanaji wa huduma bora.




-Dkt. Kijaji: Watanzania tumieni fursa kupeleka bidhaa Uingereza.

Serikali imewashauri watanzania kutumia fursa ya mpango wa biashara wa Nchi zinazoendelea kwa kuhakikisha wanapeleka bidhaa katika nchi ya Uingereza ili kukuza Uchumi pamoja na pato la Taifa.

Mpango huo mpya umeanza kutumika mwaka jana 2023 ambapo Serikali ya Uingereza iko tayari kupokea bidhaa mbalimbali zinazozalishwa nchini zikiwemo zenye kulipiwa ushuru na zisizolipiwa.

Waziri wa Viwanda na Biashara,Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji amesema hayo leo Dar es Salaam katika semina ya wafanyabiashara kuhusu fursa ya kuuza bidhaa katika soko la Uingereza na Nchi zinazoendelea (UK- DCTS).

Akizungumza Mhe.Dkt. Kijaji amesema mpango huo wa bishara na Nchi zinazoendelea kwa Tanzania umekuja muda muafaka kwa kuwa Nchi imerekebisha na kuboresha mazingira ya biashara ili kufanya kukuza kipato na biashara nchini.

Amesema kwa mwaka 2022 mauzo ya Tanzania kwenda Uingereza yalifikia sh. bil 44 ikilinganishwa na manunuzi ya sh. trilioni 3.08 ya bidhaa kutoka Uingereza.

Amesema kupitia takwimu hizo ongezeko la mauzo kwenda Uingereza ni ndogo sana ikilinganishwa na ununuzi wa bidhaa kutoka Uingereza Kwenda Tanzania kwani kwa miaka miwili imeongezeka sh. bilioni mbili wakati bidhaa zilizonunuliwa ni zenye thamani ya sh. triloni 1.06.

“Inahitaji nguvu ili kuweza kuvuka na kufikia malengo halisi ya kuanzishwa kwa mpango huo,” amesema Waziri Kijaji.

Aidha, ametolea mfano taarifa ya Kituo cha Uwekezaji nchini ( TIC) kuanzia mwaka 1997-2024 jumla ya miradi 980 ya kampuni ya Uingereza yenye thamani ya Dola za Marekani milioni 5655.38 zilizotoa ajira za wastani wa watu 126,322 katika sekta mbalimbali ziliwekezwa nchini.

“ Tuweze kutumia mpango huo na kuchochea mapato pamoja na fedha za kigeni, lakini pia kupitia mpango huo Taifa litakuwa na manufaa mbalimbali ambayo ni kupungua kwa masharti ya kupeleka bidhaa na kwa wenye viwanda ni muhimu kuwa na malighafi zitakazochochea ushindani wa bidhaa za Tanzania,” amesema.

Ameongeza pia manufaa ya mpango huo ni kupungua kwa gharama za kufanya biashara kurahisisha upatikanaji wa taarifa za masoko kwa Tanzania na hata kushirikiana na kampuni za Uingereza kuwekeza na kuzalisha bidhaa bora Tanzania.

Amehamasisha wafanyabiashara kuona umuhimu wa uadilifu katika kuziona fursa na kwamba wapeleke bidhaa zinazokidhi soko hilo.

“Serikali yetu ya awamu ya sita imechukua hatua nyingi za kujenga mahusiano ya kidipolomasia na Uingereza ambapo Nchi hiyo pia ilianza kutoa fedha kupitia huduma mbalimbali ambazo zimeelekezwa katika Miradi mbalimbali,” amesema.

Mhe. Dkt.Kijaji ameongeza kuwa mpango huo umezingatia pia sekta ya biashara kwa kuongeza mchango wa sekta ya biashara katika ukuaji wa viwanda.

Akitoa ujumbe kutoka Ubalozi wa Uingereza nchini Tanzania David Cancar amesema chini ya mpango huo Tanzania ndio yenye bidhaa zinazotakiwa na Uingereza.

Amesema kupitia mpango huo kwa Pamoja kutakuwa na ongezeko kubwa la biashara kati ya Tanzania na Uingereza.








Na Janeth Raphael -MichuziTv Dodoma

Watanzania wote waalikwa katika ibada maalum ya kumbukizi ya miaka 40 Hayati Edward Moringe Sokoine,aliyekuwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itakayofanyika Monduli juu mkoani Arusha Aprili 12,2024.

Taarifa hiyo imetolewa mapema leo hii Jijini Dodoma na Msemaji wa familia ya Hayati Sokoine Bwana Lembus Kipuyo alipokuwa akiongea na wanahabari, na kuongeza kuwa kumbukizi hii imeandaliwa na familia ikishirikiana na Taasisi ya hayat Edward Moringe Sokoine.

"Nawaalika watanzania wote kwenye ibada maalum ya kumbukizi ya miaka 40 ya Hayati Edward Moringe Sokoine, aliyekuwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, itakayofanyika Ijumaa Aprili 12, 2024, katika Kijiji cha Enguik, Monduli Juu mkoani Arusha".

"Ibada hiyo itakayofanyika siku ya Ijumaa Aprili 12, 2024, saa 3:00 asubuhi, imeandaliwa na familia ikishirikiana na Taasisi ya Hayati Edward Moringe Sokoine".

Aidha Bwana Kipuyo amesema Raisi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh Dkt Samia Suluhu Hassan atawaongoza viongozi mbalimbali wa serikali katika kumbukizi hii.

"Ibada hiyo ya kumbukumbu ya Hayati Sokoine itawashirikisha viongozi mbalimbali wa Serikali wakiongozwa na Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan".

Pia amezungumzia malengo ya kuanzishwa kwa Taasisi hiyo ya ya Hayati Edward Moringe Sokoine kuwa ni kuenzi mema aliyoyafanya katika Utumishi na enzi za uhai wake.

"Lengo kubwa la kuanzishwa kwa Taasisi ya Hayati Edward Moringe Sokoine, ni kuenzi mema aliyoyafanya, kwani aliacha alama kubwa ambayo taifa linamkumbuka hadi leo".

"Taasisi hiyo imejikita katika masuala ya elimu, kilimo, hifadhi ya mazingira, vyanzo vya maji pamoja na afya".

Sambamba na hayo yote hakuacha kuelezea uzalendo uliokuwa nao Hayati Edward Moringe Sokoine kwa taifa na wananchi kwa ujumla.

"Hayati Sokoine alikuwa mzalendo wa kweli, alipenda taifa lake na wananchi wake, alihakikisha kwamba rasilimali za nchi zinatumika na watanzania wote, aliwatumikia wananchi bila kubagua na alikuwa na hofu ya Mungu katika kufanya kazi zake".

"Hayati Sokoine alikuwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika vipindi viwili wakati wa uongozi wa Awamu ya Kwanza. Alizaliwa Agosti 01, 1934, kijijini Enguik, Monduli Juu wilayani Monduli, mkoani Arusha".



Shirika la Viwango Tanzania ( TBS ) , Leo Machi 28, 2024 limeadhimisha siku ya viwango Afrika na kutoa vyeti na zawadi kwa Washindi 10 Bora wa Mashindano ya Insha ambapo Washindi wa nafasi tano za Mwanzo (waliopewa Zawadi za Fedha Taslimu) watashiriki Mashindano ya Insha Afrika.

Akizungumza katika Hafla iyo iliyofanyika makao makuu ya TBS Jijini Dar Es Salaam, Mkuu wa Wilaya ya Ubungo Mhe. Hassan Bomboko ambaye alimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Dar Es Salaam Mhe. Albert Chalamila , amelipongeza Shirika la Viwango Tanzania kwa kazi na Jitihada kubwa za kuhakikisha Watanzania wanafikiwa na Bidhaa zilizo Bora hasa katika kipindi hiki cha Miaka Mitatu ya Serikali ya awamu ya SITA inayooongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

" Niwapongeze TBS kwa kuadhimisha siku hii muhimu kwa namna ya Kitofauti lakini pia niwapongeze washiriki wote zaidi ya 300 waliojitokeza kushiriki mashindano ya Insha hadi sasa tumewapata 10 bora , nyinyi kama wataalamu wetu wa badae wa masuala ya Viwango mmefanya jambo kubwa sana , Juzi wakati tukiadhimisha miaka mitatu ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan TBS ni moja kati ya Mashirika yaliyofanya vizuri niwapongezeni sana " alisema Mhe. Bomboko

Akitoa Historia ya Siku ya Viwango Afrika , Mkurugenzi Mkuu TBS , Dkt. Athuman Ngenya amesema
" Shirika la Viwango Afrika lilianzishwa mwaka 1977 likiwa na jukumu kuu la Kuoanisha viwango Afrika ili kukuza biashara na kupunguza vikwazo vya Kibiashara barani Afrika pamoja na kuimarisha ukuaji wa Viwanda Afrika .





Na Khadija Kalili, Michuzi Tv
ASKARI wawili wa Jeshi la Zimamoto na uokoaji wamejeruhiwa wakiwa katika harakati za kuokoa marehemu waliokuwa wamenasia kwenye gari baada ya kuzuka moto ghafla na magari kuwaka moto .

Hayo yamesemwa leo Machi 28 na Kamanda wa Polisi Mkoa Mkoa wa Pwani (SACP) Pius Lutumo alipozungumza na Waandishiwa Habari.

RPC Lutumo amewataja askari waliojeruhiwa kuwa ni Koplo Elias Bwire na Koplo Hamisi Kungwi wote wamekimbizwa Hospitali ya Taifa Mloganzila kwa matibabu na hali zao zinzendelea vizuri.

" Machi 28 mwaka huu majira ya saa 10:15 alfajiri katika bonde la Ruvu Wilaya ya Kipolisi Mlandizi, Mkoa wa Pwani barabara ya Morogoro, Dar es Salaam gari namba T668 DTF aina ya Scania Kampuni ya Sauli ikiendeshwa na dereva Idd Aloyce (35),mkazi wa Mafinga ikitokea Dar es Salaam kwenda Mbeya liligonga ubavuni lori la mafuta ya Petroli lenye namba za usajiri RAF672N na tela lenye namban RL2594 aina ya Howo lililokuwa linatoka Dar es Salaam kwenda nchini Rwanda likiendeshwa na dereva Mushimana Musiyimana lililokuwa limesimama kupisha gari lililokuwa linakuja mbele yake".

Aidha basi hilo lilikuwa limeongozana na basi la Golden Deer Kampuni ya New Force lenye namba za usajiri RAF672N na likiendeshwa na dereva aitwaye Burton Jacob (33),.mkazi wa Mbeya ambapo nalo lililigonga kwa nyuma basi la Saul lililokuwa mbele yake na kusababisha vifo vya watu wawili ambao hawakufahamika majina yao na majeruhi watatu ambao ni Salimu Daud (50) mkazi wa Mbozi Mbeya, Farida Idrisa (26)mkazi wa Tabata Dar es Salaam na Kiambile Geofrey mkazi wa Uyole Mbeya.

RPC Lutumo chanzo cha ajali hiyo ni uzembe wa madereva wa mabasi yote mawili kushindwa kuchukua tahadhari kwa kuyapita magari mengine lakini pia kushindwa kutunza umbali kati ya gari moja na lingine huku yakiwa yamefatana.

"Pamoja na hayo uchunguzi wa awali unaonesha kuwa chanzo cha moto huo ni hitilafu ya injini ya basi la Saul iliyokua imekita chini baada ya kugonga gari lingine na kuripua petroli wakati wa uokoaji"amesema RPC Lutumo.

"Wito wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Pwani unawataka madereva kutii sheria za Usalama Barabarani kwa mujibu wa taaluma zao na ifahamike kwamba madereva wanachukua dhamana kubwa ya maisha na mali za watu"

Mkuu wa mkoa wa Pwani Abubakari Kunenge amesema atayafungia mabasi yatakayoendelea kuvunja Sheria za Usalama Barabarani baada ya ajali iliyotokea alfajiri ya leo.

RC Kunenge amesema hayo wakati akizungumza na Waandishi wa Habari Ofisini kwake Kibaha Mkoani Pwani, amesema yeye ameamua kwa kushirikiana na wanaotoa lesseni, LATRA na Jeshi la Polisi kuwa wataweka mkakati wa kudhibiti ajali ndani ya Mkoa wa Pwani.

" Mtagundua kuwa Mkoa wa Pwani hii Barabara ni kubwa na mabasi yakitoka kule stendi kuu ya Dar es salaam Mbezi idadi ya mabasi ni mengi yakiwa yamekaguliwa lakini bado hapa pia tunakagua " amesema.
















Top News