Na Veronica Simba – Sikonge
 Imeelezwa kuwa nishati ya umeme kwa wananchi sasa ni muhimu sawa na ilivyo kwa chakula. 
Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dkt Medard Kalemani aliyasema hayo kwa nyakati tofauti hivi karibuni (Julai 27), katika vijiji vya Kiloleli na Mole, wilayani Sikonge mkoani Tabora, alipokuwa katika ziara ya kazi kukagua utekelezaji wa miradi ya umeme vijijini awamu ya pili maarufu kama REA II.

Akifafanua kuhusu ulinganifu wa umeme na chakula kwa wananchi, Dkt Kalemani alieleza kuwa, mwananchi anayepata umeme, ana uhakika wa kuishi maisha mazuri yanayojumuisha afya njema na maendeleo kwa kila nyanja. 
“Bila umeme, hakuna maendeleo kwa jamii. Huduma zote muhimu kwa binadamu, ili ziwe katika viwango stahiki, zinahitaji umeme. Afya, elimu, biashara na vingine mvijuavyo, vinahitaji umeme ili vifanyike kwa ubora. Hivyo basi, kama ilivyo muhimu kwa binadamu kupata chakula ili aishi, ndivyo ilivyo muhimu kuwa na umeme ili kuwa na uhakika wa maisha bora,” alisisitiza. 
Dkt Kalemani alieleza kuwa, kutokana na umuhimu huo wa nishati ya umeme kwa wananchi, Serikali inatekeleza miradi mbalimbali ukiwemo wa Umeme Vijijini (REA) ili kuhakikisha huduma hiyo muhimu inapatikana kwa watanzania wote hata wale walio vijijini.

Aidha, alisema kwamba, Serikali haitasubiri mtu ajenge nyumba ya kiwango fulani ndipo aunganishiwe umeme bali kila mwananchi ataunganishiwa huduma hiyo hata kama nyumba yake ni duni. 
“Serikali inatambua kuwa siyo kila Mtanzania ana uwezo wa kujenga nyumba bora kwa kuwa tunatofautiana kipato. Hivyo, nyumba duni haitakuwa sababu ya kuzuia mwananchi husika kuunganishiwa umeme. Zoezi la kuunganisha umeme litaendelea wakati wananchi wakiendelea kuboresha makazi yao ili umeme uwasaidie kuinua vipato vyao.”

Kuhusu suala la vijiji ambavyo havikuunganishiwa umeme katika Mradi wa REA Awamu ya Pili, Naibu Waziri alieleza kuwa vijiji hivyo vyote vitapatiwa umeme katika Awamu ya Tatu (REA III) ya Mradi husika ambayo inatarajiwa kuanza rasmi utekelezaji wake mwezi Septemba mwaka huu.

Alisema kuwa, uzoefu uliopatikana kutokana na utekelezaji wa Mradi wa Umeme Vijijini Awamu ya Pili umebainisha kuwa hakukuwa na ushirikiano mzuri baina ya wasimamizi wa Mradi na viongozi mbalimbali katika ngazi za Wilaya, Halmashauri na Vijiji ambako Mradi husika ulikuwa ukitekelezwa, hali iliyosababisha baadhi ya maeneo muhimu kurukwa pasipo kupatiwa huduma hiyo. 
Naibu Waziri alieleza kuwa, kutokana na uzoefu huo, Serikali imedhamiria, katika Awamu ya Tatu ya Mradi, kuwashirikisha ipasavyo, viongozi katika ngazi hizo, ambao ndiyo wanafahamu vema maeneo yao ili wabainishe maeneo ya vipaumbele kwa ajili ya kupatiwa nishati ya umeme.

Katika hatua nyingine, Dkt Kalemani aliwataka watendaji wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), kuendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu huduma mbalimbali zinazotolewa na shirika hilo ili kuwaepusha wateja wao kutapeliwa na matapeli maarufu kama ‘vishoka’ ambao hutumia fursa ya uelewa mdogo wa wananchi. 
Miongoni mwa mambo muhimu ambayo Naibu Waziri aliagiza wananchi wapewe elimu ni pamoja na umuhimu wa kutunza miundombinu ya umeme na bei halisi ya umeme wa REA. 
Alitoa onyo kwa wale wanaohujumu miundombinu ya umeme kuwa hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yao endapo watabainika kufanya hivyo kwani wanarudisha nyuma jitihada za Serikali kuwaletea wananchi wake maendeleo. 
Naibu Waziri anatarajia kuhitimisha ziara yake mwishoni mwa mwezi huu katika Mkoa wa Geita. Mikoa ambayo amekwishaitembelea katika ziara hiyo ni Dodoma, Iringa, Rukwa, Katavi na Tabora.
 Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Tabora ambaye pia ni Katibu Tawala wa Mkoa huo, Thea Ntala akizungumza na wananchi wa eneo la Kiloleli wilayani Sikonge mkoani humo hivi karibuni wakati wa ziara ya Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dkt Medard Kalemani kukagua utekelezaji wa Mradi wa REA Awamu ya Pili.
 Mbunge wa Sikonge, George Kakunda (kushoto) akimweleza jambo Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dkt Medard Kalemani (katikati), wakati wa ziara ya Naibu Waziri wilayani humo hivi karibuni kukagua utekelezaji wa Mradi wa REA Awamu ya Pili. Kulia kwa Naibu Waziri ni Mkuu wa Wilaya ya Sikonge, Peres Magiri.
 Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dkt Medard Kalemani (wa pili kutoka kushoto) akiwakabidhi viongozi wa Wilaya ya Sikonge, kifaa kinachotumika kuunganisha umeme pasipo kutumia nyaya za kawaida za kuunganishia kijulikanacho kitaalam kama ‘Ready Board’ au UMETA (Umeme Tayari), wakati akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Kiloleli wilayani humo hivi karibuni.
Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dkt Medard Kalemani (kushoto), akikagua mtambo unaotumika kusukuma maji kwa ajili ya matumizi ya wakazi wa Wilaya ya Sikonge mkoani Tabora hivi karibuni. Mtambo huo uliopo katika eneo la Utyatya, hutumia mafuta ya dizeli ambayo ni gharama kubwa. Eneo hilo ni mojawapo ya maeneo yanayotarajiwa kuunganishiwa umeme wa REA Awamu ya Tatu na hivyo kuondoa kabisa changamoto hiyo. Katikati ni Mkuu wa Wilaya ya Sikonge, Peres Magiri.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...