Na Mwandishi Wetu, Dodoma

MKUTANO Mkuu wa Mwaka wa Vyombo vya Utangazaji 2026 umeanza rasmi jijini Dodoma kwa mijadala mizito inayolenga kuimarisha sekta ya utangazaji nchini. Mkutano huo wa siku mbili ulioanza leo Februari 12, 2026 unatarajiwa kuhitimishwa kesho Februari 13, 2026.

Mkutano huo umeandaliwa na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) ukishirikisha wadau mbalimbali wa sekta ya habari wakiwemo wamiliki wa televisheni, redio na majukwaa ya mitandao ya kijamii kutoka maeneo mbalimbali ya nchi.

Akiwasilisha mada ya kwanza, Mhandisi Andrew Kisaka kutoka TCRA alizungumzia matokeo na utekelezaji wa mapendekezo yaliyotokana na utafiti wa huduma za utangazaji nchini. Alieleza hatua zilizochukuliwa kuboresha ubora wa maudhui, kuimarisha usimamizi wa leseni pamoja na kuzingatia weledi katika utoaji wa taarifa kwa umma.

Wasilisho la pili lilitolewa na Mhadhiri Msaidizi Zuhura Selemani ambaye alielezea fursa na faida za uwekezaji wa teknolojia katika utangazaji vijijini. Alisisitiza umuhimu wa kutumia teknolojia za kisasa kufikisha taarifa kwa wananchi wa maeneo ya pembezoni na kuongeza ushiriki wao katika maendeleo ya taifa.

Kwa upande wake, Nancy Mwaisaka kutoka UNESCO aliwasilisha mada kuhusu TEHAMA na huduma za utangazaji wa redio vijijini, akitoa uzoefu wa taasisi hiyo katika kusaidia redio za kijamii. Alibainisha kuwa redio za vijijini zina mchango mkubwa katika kuelimisha jamii na kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Washiriki wa mkutano huo wanatarajiwa kujadili kwa kina changamoto na fursa zilizopo katika sekta ya utangazaji, huku wakitoa mapendekezo yatakayosaidia kuboresha mazingira ya kazi na kulinda maslahi ya umma katika upatikanaji wa taarifa sahihi na kwa wakati.




 

SERIKALI imetangaza neema ya kihistoria kwa wanablogu, vijana wabunifu, na watoa maudhui mtandaoni nchini kwa kupunguza ada za leseni kwa kiwango kikubwa, hatua inayolenga kuchochea ukuaji wa uchumi wa kidijitali na kurasimisha shughuli za wahabarishaji wa mitandao.

Hatua hiyo imekuja kufuatia utafiti wa kina na mikutano ya kimkakati ya takribani mwaka mzima kati ya mtandao wa Tanzania Bloggers Network (TBN) na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), ikielezea vikwazo vya gharama vilivyokuwa vikikwaza uandishi wa habari za kidijitali nchini.
Akizungumza katika ufunguzi wa Mkutano wa Mwaka wa Watoa Huduma za Utangazaji (ABC 2026) jijini Dodoma leo, Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Hamisi Mwinjuma, amesema ada ya leseni kwa watoa maudhui mtandaoni imeshushwa kutoka Sh500,000 hadi Sh50,000 tu, huku ada ya maombi ikiwa ni Sh10,000 pekee.

Mageuzi hayo pia yamegusa kundi la wakusanyaji wa maudhui (Online Content Aggregators), ambao ada yao imeshushwa kutoka Sh1,000,000 hadi Sh100,000 pekee. Aidha, kundi la "Amateteur" limeanzishwa kwa ajili ya vijana wanaochipukia ili waweze kujitambulisha rasmi na kukuza vipaji vyao bila vikwazo vya kifedha.

Mapinduzi ya Teknolojia ya DSB
Wakati neema hiyo ikitangazwa, Mkurugenzi Mkuu wa TCRA, Dkt. Jabiri Bakari, ametangaza kuanza kwa teknolojia mpya ya utangazaji wa redio ya kidijitali nchini inayojulikana kama Digital Sound Broadcasting (DSB).

Teknolojia hiyo itaanza kufanya kazi katika mikoa mitano ya majaribio ya Dar es Salaam, Dodoma, Mwanza, Arusha, na Mbeya, lengo likiwa ni kuongeza ubora wa sauti na huduma za utangazaji nchini.

"Tumekamilisha maandalizi yote ya kiudhibiti na watoa huduma wa miundombinu wameshapatikana. Hii ni hatua kubwa ya kuendana na mabadiliko ya teknolojia duniani na kuimarisha utangazaji, hususan maeneo ya vijijini," alisema Dkt. Bakari.

Utafiti: Redio Bado ni Kinara
Katika mkutano huo, Injinia Andrew Kisaka wa TCRA amewasilisha matokeo ya utafiti wa hali ya utangazaji kwa mwaka 2025/2026, ukionyesha kuwa redio inaendelea kuwa chanzo kikuu cha habari kwa asilimia 85 ya Watanzania. Hata hivyo, utafiti huo umebaini ukuaji mkubwa wa matumizi ya intaneti miongoni mwa vijana, ambapo asilimia 45 hupata habari kupitia mitandao ya kijamii kabla ya kusikiliza redio au kutazama televisheni.

Upande wa televisheni, utafiti unaonyesha asilimia 65 ya watazamaji wanatumia ving'amuzi, huku maudhui ya ndani yakipendwa zaidi kwa asilimia 70. Serikali imewahimiza watoa huduma za kienyeji kuwekeza zaidi kwenye majukwaa ya kidijitali (OTT) ili kukidhi mahitaji ya soko la sasa.

Ulinzi wa Hakimiliki na Mikopo
Ili kuhakikisha wanahabari wa kidijitali wanufaika na kazi zao, Serikali imezielekeza taasisi za COSOTA na TCRA kuandaa mpango wa kulinda hakimiliki na kudhibiti uharamia mtandaoni. Aidha, Serikali imeanza kutoa mikopo ya masharti nafuu kwa watengeneza maudhui kwa ajili ya ununuzi wa vifaa vya kisasa vya kufanyia kazi.

Hadi kufikia Desemba 2025, TCRA imetoa jumla ya leseni 707 za utangazaji, zikiwemo 318 za maudhui mtandaoni, jambo linaloashiria kukua kwa uhuru wa habari na demokrasia nchini chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan.










 

Manyoni, Singida, Februari 12, 2026 — Ziara ya mafunzo ya wataalamu wa Idara ya Misitu Zanzibar imeingia siku ya pili leo kwa ujumbe huo kuanza rasmi mafunzo ya vitendo katika Shamba Darasa la Nyuki la TFS, wilayani Manyoni.

Mafunzo hayo yameanza kwa mada ya uanzishaji na usimamizi bora wa Hifadhi za Nyuki (Bee Reserves) iliyowasilishwa na Askari wa Uhifadhi – Ufugaji Nyuki Wilaya ya Manyoni, Jacline Leshabari, akieleza hatua za kisheria, kiutawala na kiikolojia zinazohitajika katika kuanzisha na kulinda maeneo maalum ya nyuki.

Akiwasilisha mada hiyo, Leshabari amesema hifadhi za nyuki zimekuwa nyenzo muhimu si tu katika kuongeza uzalishaji wa asali na mazao yatokanayo na nyuki, bali pia katika kulinda misitu na bioanuai. “Usimamizi madhubuti wa hifadhi hizi unahakikisha upatikanaji endelevu wa malighafi za nyuki huku ukihifadhi mfumo wa ikolojia,” amesema.

Kwa mujibu wa ratiba ya mafunzo, wataalamu hao kutoka Zanzibar wanatarajiwa pia kujionea kwa vitendo utambuzi wa maeneo ya hifadhi, uwekaji wa mizinga ya kisasa, pamoja na mbinu za kushirikisha jamii katika kulinda na kunufaika na rasilimali za nyuki.

Mkurugenzi wa Idara ya Misitu Zanzibar, Said Juma Ali, amesema mafunzo ya siku ya pili yamewapa mwanga mpana juu ya namna TFS inavyounganisha uhifadhi na uchumi wa jamii kupitia sekta ya nyuki. Amesisitiza kuwa uzoefu huo utasaidia Zanzibar katika mpango wake wa kuanzisha hifadhi za nyuki na kuendeleza utalii wa nyuki.

Ziara hiyo ya siku tano inatarajiwa kuendelea kwa mafunzo zaidi kuhusu uchakataji wa asali, viwango vya ubora na masoko, huku ushirikiano kati ya TFS na Idara ya Misitu Zanzibar ukitajwa kuwa kichocheo cha mageuzi ya sekta ya nyuki nchini.




 

Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Elimu Tanzania Dkt. Aneth Komba amesema, Serikali imetoa vitabu vya masomo ya Elimu ya Amali bure kwa shule zote za umma na binafsi ili kuongeza hamasa katika ufundishaji na ujifunzaji wa masomo hayo yatayosaidia kukabiliana na changamoto ya ajira kwa mwanafunzi pindi wanapohitimu.

Dkt. Komba amesema hayo leo Februari 12, 2026 katika zoezi la ugawaji wa vitabu vya Amali kwa wakuu wa shule zote Tanzania Bara ambazo zinatoa Elimu ya Sekondari katika mkondo huo.

Amesema, mwaka 2024 Serikali ilianza kutekeleza Mtaala uliobereshwa ambao umegawanyika katika mkondo wa Amali na mkondo wa jumla, huku akisisitiza mkondo wa Amali lengo lake ni kujenga Elimu ujuzi kwa mwanafunzi.

Sambamba na ugawaji wa vitabu vya Amali, Dkt. Komba amesema, TET imetoa mafunzo kwa wakuu wa shule wote kuhusu maboresho yaliyofanyika kwenye Mtaala hasa katika mkondo wa Amali, pamoja na namna kutumia Maktaba mtandao ambapo vitabu vyote hupatikana.

Aidha, Dkt Komba amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha zilizosaidia upatikanaji wa vitabu nchini, hasa vitabu vya Amali ambavyo vinagawiwa bure kwa shule zote nchini za Serikali na za binafsi.

Nae, Meneja uchapaji na usambazaji wa vitabu Taasisi ya Elimu Tanzania Bw. Emmanuel Stanslaus ametoa wito kwa walimu kuhakikisha wanatua vitabu hivyo kwa usahihi ili vilete tija kwa wanafunzi kulingana na fani wanazosoma.

Kwa upande wake Mkuu wa shule ya ufundi Nzega na Makamu Mwenyekiti wa wakuu wa shuke Tanzania Bara Mwl. Mwanakombo Juma Martin amesema vitabu hivyo vilivyotolewa bure kwa shule za Serikali na binafsi vitasaidia katika ufundishaji na ujifunzaji kwa wanafunzi hivyo kuleta tija katika utekelezaji wa Mtaala ulioboreshwa mkondo wa Amali.

Nae, Mkuu wa shule ya Ufundi ya wavulana Bwiru iliyopo Mkoani Mwanza Mwl. Thomas Werema amesema Elimu ya Amali inaenda kuwa Mkombozi kwa vijana wa Tanzania, kwani hutoa fursa kwa mw anafunzi kujiajiri, kuajiriwa au kuajiri wengine pindi amalizapo masomo yake, hivyo kusaidia kukabiliana na changamoto ya ajira nchini.












Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Kanali Yahya Ramadhani Kido, Februari 12, 2026 ametembelea Ofisi za Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Kagera kwa lengo la kujitambulisha na kusalimiana na viongozi wa chama ngazi ya mkoa na wilaya.

Ziara hiyo imefanyika siku moja baada ya Kanali Kido kuwasili mkoani Kagera kufuatia uteuzi wake wa hivi karibuni kuwa Mkuu wa Mkoa huo. Katika ziara hiyo, aliambatana na Katibu Tawala wa Mkoa wa Kagera, Bw. Stephen Ndaki, pamoja na Mkuu wa Wilaya ya Bukoba, Mwl. Erasto Sima.

Kanali Kido alipokelewa katika ofisi hizo na Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Mkoa wa Kagera, Ndg. Kareem Amri (MNEC), kwa niaba ya Mwenyekiti wa CCM Mkoa na viongozi wengine wa chama.

Akizungumza wakati wa salamu za utambulisho, Kanali Kido alimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM Taifa, kwa kumuamini na kumteua kushika wadhifa huo.

Ameahidi kutoa ushirikiano wa dhati katika kutekeleza majukumu yake kwa kuzingatia maelekezo na dira ya Mheshimiwa Rais ya kuwahudumia wananchi kwa ufanisi.

Kwa upande wake, Ndg. Kareem Amri alimpongeza Kanali Kido kwa uteuzi huo na kumtakia mafanikio katika majukumu yake mapya. 

Aidha, alimkabidhi Ilani ya CCM inayobainisha ahadi na vipaumbele vilivyokusudiwa kutekelezwa katika Mkoa wa Kagera, akimtaja Mkuu wa Mkoa kuwa msimamizi mkuu wa utekelezaji wa ilani hiyo ngazi ya mkoa.

Ziara hiyo imeelezwa kuwa ni sehemu ya utaratibu wa kuimarisha ushirikiano kati ya Serikali na Chama katika kusimamia na kutekeleza mipango ya maendeleo kwa manufaa ya wananchi wa Kagera.





 

Na Seif Mangwangi, Michuzi TV, Arusha.

Taasisi ya waandishi wa habari ya kusaidia jamii za pembezoni(MAIPAC) imetoa mafunzo kwa waandishi wa habari nchini jinsi ya kuandika habari zinazochochea amani na kulinda usalama wao wakati wa migogoro.

Mafunzo hayo yameshirikisha waandishi wa habari kutoka mikoa ya Dar es Salaam,Mwanza,Geita,Mara,Manyara,Mbeya na Arusha,yalidhaminiwa na shirika la wanahabari la Press Unlimited.

Akifungua mafunzo hayo,Mkurugenzi wa MAIPAC, Mussa Juma aliwataka wanahabari kuandika habari ambazo zinahamasisha amani wakati wa migogoro na kuhakikisha wanakuwa salama.

Juma alisema, habari za upande mmoja ambazo hazizingatii maadili na maslahi mapana ya Umma zimekuwa zikisababisha migogoro katika jamii.

Hata hivyo,aliwataka wanahabari wakati wote wa kazi zao kuzingatia usalama wao,kufanya upembuzi yakinifu wa habari wananayotaka kuandika kabla ya kuandika na baada ya kuandika.

"Tujuwe habari ina madhara gani,inafaida gani ,tusiwe na upande katika hiyo habari na kubwa tuwe tunachukuwa tahadhali za kiusalama wa tunapotumia vyombo vya kidigitari na usalama binafsi"alisema

Wakili  wa kujitegemea John Sendodo akitoa mafunzo kuhusu sheria mbalimbali za masuala ya habari ,aliwataka wanahabari kuzingatia sheria hizo hata kama.zinamapungufu.

"Kuna sheria kadhaa ambazo lazima mzijuwe ikiwepo sheria ya huduma za habari ya mwaka 2016 ,sheria ya makosa ya mitandaoni ya mwaka 2015,kanuni.za maudhui mitandao na nyingine kadhaa tusome tujuwe"alisema

Wakili.Sendodo ambaye anafanyakazi na shirika la.kimataifa la Protection Afrika  akifafanua sheria hizo,vifungu kwa vifungu pamoja na mikataba kadhaa ya kimataifa lnayohusiana na wanahabari aliwataka wanahabari kufanyakazi kwa kutovunja sheria lakini wakitekeleza wajibu wao "alisema.

Mmiliki wa Chuo cha waandishi wa habari cha Fanikiwa kilichopo Arusha,Mwanahabari Joseph Mayagilla akitoa mada katika mafunzo hayo, aliwataka wanahabari wakati wote wa kazi zao kuzingatia maadili ya uandishi.

Mayagilla alisema habari za upande mmoja.zimekuwa na madhara katika jamii na sasa kumeibuka uandishi usiojali maadili ya uandishi.

Hata hivyo, alisema ili kuhakikisha habari.zinakuwa bora ni muhimu kurejesha madawati ya vitengo kadhaa kwenye vyombo vya habari ikiwepo madawati ya habari za uchunguzi,amani na maendeleo,uchumi na mengine kwani yataongozwa na waandishi wabobezi wa eneo husika.

Mtaalam wa masuala ya Saikolojia,Ester Cornelio aliwataka wanahabari wanaokabiliwa na msongo wa mawazo kutojifungia kwenye vyombo vya habari na watoke kupata tiba.

Alisema kunywa pombe kupita kiasi ama kuvuta sana sigara hakuwepo kuondoa Msongo wa mawazo (trouma) bali ni kufika kwa wataalam na kupata tiba ambayo ni ushauri.

Cornelio alisema wanaume wamekuwa wahanga wa msongo wa mawazo ama sonona kwa sababu hawazungumzi ili kutoa yaliyomoyoni tofaufi na wanawake.

Wakichangia mada katika mafunzo hayo, Wanahabari Tausi Mbowe ambaye ni meneja wa dawati ya Kidigitali Star Tv,  na Anthony Mayunga kutoka serengeti media, walieleza umuhimu wa maadili ya uandishi na athari za msongo wa mawazo na mapungufu ya sheria.

Tausi Mbowe alishauri kuendelea kuimarishwa mafunzo ya mara kwa mara kwa wanahabari hasa kuhusiana na sheria na kukabiliana na msongo wa mawazo.

Upande wake mwanahabari Elizabeth Nyivambe kutoka Mbeya na Muta Robet wa Geita na Zakaria Mtigandi wa Manyara walieleza pia umuhimu wa kuendelezwa mafunzo hasa masuala ya matumizi sahihi ya mitandao na usalama kwa wanahabari.







Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni akizungumza wakati wa semina kuhusu Muungano na Mazingira kwa wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iliyofanyika katika Ukumbi wa Pius Msekwa jijini Dodoma, Februari 11, 2026.

*************

Na; Mwandishi Wetu, Dodoma

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni ametoa rai kwa wabunge kupinga na kusahihisha upotoshaji wa taarifa kuhusu Muungano, hususan kupitia mikutano ya hadhara na mitandao ya kijamii.

Ametoa rai hiyo wakati wa semina kuhusu Muungano na Mazingira kwa wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iliyofanyika katika Ukumbi wa Pius Msekwa jijini Dodoma, Februari 11, 2026.

Mhandisi Masauni amesema kuwa Muungano una faida nyingi hivyo ni wakati sasa wabunge kusikiliza na kuwasilisha kwa busara hoja za wananchi kuhusu Muungano

Amesisitiza kuwa wabunge ni nguzo muhimu ya kulinda na kuimarisha Muungano wa Tanzania na wanabeba dhamana ya kihistoria ya kuhakikisha Muungano unaendelea kuwa chanzo cha amani, mshikamano na maendeleo ya Taifa.

Kwa upande wa mazingira, amesema Ofisi ya Makamu wa Rais kwa kushirikiana na wadau imeandaa Programu ya Mageuzi ya Kukijanisha Tanzania ikiwa na lengo la kuleta mageuzi jumuishi na shirikishi yenye matokeo makubwa yanayolenga kuimarisha uhimilivu wa mabadiliko ya tabianchi kwa kuongeza eneo lenye uoto wa kijani kupitia upandaji miti.

Mhe Masauni amesema Julai 17, 2025 Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan alizindua Dira 2050 ambayo imetambua na kuweka nguzo mahususi ya hifadhi na ustahimivu wa mabadiliko ya tabianchi.

“Serikali kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais kwa kushirikiana na wadau imeandaa Programu ya Mageuzi ya Kukijanisha Tanzania ikiwa na lengo la kuleta mageuzi jumuishi na shirikishi yenye matokeo makubwa yanayolenga kuimarisha uhimilivu wa mabadiliko ya tabianchi kwa kuongeza eneo lenye uoto wa kijani kupitia upandaji miti.

“Kwa kuzingatia Dira 2050 imeelekeza Tanzania kuwa kinara barani Afrika katika masuala ya hifadhi na usimamizi wa mazingira, programu ambayo itawasilishwa kwa wabungeitazingatia masuala Uhifadhi wa ardhi oevu, Matumizi ya nishati safi ya kupikia, upandaji miti, biashara ya kaboni, udhibiti wa taka na usafi wa mazingira na udhibiti wa viumbe vamizi,” amesema Mhe. Masauni.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati ya kudumu ya Bunge ya Maji na Mazingira Mhe. Jackson Kiswaga amesema kupitia semina hiyo wamepata uelewa mklubwa kuhusu masuala ya mazingira.

Ameahidi kuwa pamoja na wabunge wenzao wataendelea kuwa mabalozi wazuri kwa wananchi katika kuwafundisha kuhusu uhifadhi wa mazingira endelevu.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni akizungumza wakati wa semina kuhusu Muungano na Mazingira kwa wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iliyofanyika katika Ukumbi wa Pius Msekwa jijini Dodoma, Februari 11, 2026.



Baadhi ya Wabunge wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakiwa katika semina kuhusu masuala ya Muungano na Uhifadhi wa Mazingira iliyotolewa na Ofisi ya Makamu wa Rais, katika Ukumbi wa Pius Msekwa Bungeni Dodoma, Februari 11, 2026.
Mbunge wa Viti Maalumu kundi la Wafanyakazi Mhe. Lucy Mwakyembe kutoka MkoaMjini Unguja akichangia katika semina kuhusu masuala ya Muungano na Uhifadhi wa Mazingira iliyotolewa na Ofisi ya Makamu wa Rais, katika Ukumbi wa Pius Msekwa Bungeni Dodoma, Februari 11, 2026.

PICHA NA OFISI YA MAKAMU WA RAIS
NA EMMANUEL MBATILO, MICHUZI TV

Shirika la Viwango Tanzania (TBS) limeshiriki katika Maonesho ya Biotechnology yaliyofanyika katika Ofisi za Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH), jijini Dar es Salaam, yakilenga kutoa elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa viwango.

Akizungumza katika maonesho hayo, Februari 12, 2026 Jijini Dar es Salaam, Afisa Mdhibiti Ubora wa TBS, Neema Kirway, amesema shirika hilo limeshiriki kikamilifu ili kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu jukumu la TBS katika kudhibiti ubora na usalama wa chakula pamoja na bidhaa nyingine.

Amesema TBS tayari imeanzisha viwango 74 vya Biotechnology, hatua inayolenga kulinda afya, usalama na maslahi ya Mtanzania.

“Kupitia viwango hivi, TBS itahakikisha kuwa bidhaa zote za Biotechnology zinakidhi ubora na usalama kabla ya kumfikia mtumiaji,” amesema Kirway.

Aidha, amebainisha kuwa shirika hilo liko katika mchakato wa kuandaa viwango vingine vya Biotechnology, ambavyo vipo katika hatua za mwisho kabla ya kutangazwa rasmi.

Kirway ametoa rai kwa wadau na wananchi kufahamu kuwa viwango hivyo vinapatikana na vinauzwa katika Makao Makuu ya TBS.

Amesisitiza kuwa TBS itaendelea kusimamia kikamilifu utekelezaji wa viwango ili kuhakikisha bidhaa zote zinazosajiliwa na kupitishwa na shirika hilo ni salama kwa matumizi ya binadamu.

Katika ufafanuzi wake, Kirway amesema teknolojia ya Biotechnology ina mchango mkubwa katika sekta mbalimbali ikiwemo afya, kilimo, viwanda na usalama wa chakula.

“Elimu iliyotolewa katika maonesho haya inasisitiza umuhimu wa wanasayansi kushirikiana, kubadilishana uzoefu na kuimarisha matumizi ya teknolojia na Biotechnology kwa maendeleo ya taifa,” ameongeza.

Kauli mbiu ya maonesho hayo ilikuwa: “Biotechnology Kuimarisha Usalama wa Chakula na Maendeleo ya Jamii na Uchumi.”









Top News