Na Mwandishi Wetu, Handeni TC

Madiwani wa Halmashauri ya Mji Handeni wameaswa kuzingatia miiko ya viongozi wa umma na kudumisha uadilifu katika utekelezaji wa majukumu yao.

Akizungumza katika hafla ya ufunguzi wa Baraza la Madiwani Desemba 4, 2025, kwenye ukumbi wa Halmashauri ya Mji Handeni, Bakari Mussa kutoka Ofisi ya Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma amewataka madiwani hao kuzingatia maadili, kuepuka mgongano wa maslahi, na kushirikiana kikamilifu na Mkurugenzi wa Halmashauri katika kusimamia shughuli za maendeleo.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Handeni, Maryam Ukwaju, amewahimiza madiwani kufanya kazi kwa kuzingatia maslahi mapana ya nchi na ya Halmashauri.

Amesisitiza umuhimu wa uwajibikaji na kujiepusha na vitendo vinavyohatarisha uadilifu wa utumishi wa umma.

Viongozi wa kata ya Kalangalala katika halmashauri ya manispaa ya Geita leo Disemba 04, 2025 wamempokea diwani wa kata hiyo Reuben Sagayika katika hafla fupi iliyohudhuriwa na wenyeviti wa mitaa ya kata hiyo, wakuu wa idara za elimu, afya na maendeleo ya Jamii na baadhi ya walimu wa shule zilizopo katika kata hiyo.

Hafla ya mapokezi imefanyika katika ofisi za kata hiyo zilizopo halmashauri ya manispaa ya Geita, akitoa taarifa ya maendeleo ya kata kwa kipindi cha mwezi Julai hadi Novemba mwaka wa fedha 2025/2026, Afisa mtendaji wa kata ya Kalangalala Bw. Emmanuel Bomani amesema wamefanikiwa kusajili wakulima 86 katika mfumo ili kuwawezesha kupata mbolea za ruzuku huku Diwani mstaafu Prudence Temba akiahidi kuendelea kutoa ushirikiano.

Akizungumza mara baada ya kukabidhiwa rasmi ofisi Reuben Sagayika ameeleza kuwa atafanya ziara ya kutembelea mitaa yote 11 ya kata hiyo na kuzungumza na wananchi juu ya kero na masuala mbalimbali kwa maendeleo ya kata.



Na Pamela Mollel,Arusha

Jiji la Arusha limezindua rasmi Mkutano wa Kwanza wa Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Jiji, hatua muhimu inayofungua ukurasa mpya wa uongozi na utawala katika jiji hilo. Uzinduzi huo umefanyika leo katika ukumbi wa Mkuu wa Mkoa wa Arusha, ukihusisha shughuli zote za kikatiba ikiwemo uapisho wa madiwani, uchaguzi wa viongozi na uteuzi mbalimbali.

Katika uchaguzi uliofanyika, Maxmilian Matle Iranqhe amechaguliwa kuwa Meya wa Jiji la Arusha kwa ushindi wa kishindo baada ya kupata kura 33 kati ya kura 34, huku kura moja ikiwa ya hapana. Naye Julius W. Sekeyan (CCM) ameibuka kidedea katika nafasi ya Naibu Meya, akivuna kura 31 dhidi ya mpinzani wake Stanley Nathan (NLD) aliyepata kura 3. Matokeo hayo yametangazwa na Mwenyekiti wa muda wa uchaguzi, Katibu Tawala wa Wilaya ya Arusha, Dk. Jacob Rombo, ambaye alithibitisha kuwa jumla ya madiwani 34 walipiga kura.

Mara baada ya zoezi la uchaguzi kukamilika, madiwani wote 34—wakiwemo 25 wa kuchaguliwa na 9 wa viti maalum—waliapishwa kama sharti la kisheria linalowaruhusu kuanza kutekeleza majukumu yao rasmi. Uapisho huo umeweka msingi thabiti wa kuanza kwa awamu mpya ya utawala ndani ya jiji.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mkuu wa Wilaya ya Arusha, Mhe. Joseph Modest Mkude, amewataka madiwani kufanya kazi kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za halmashauri pamoja na kutekeleza kiapo chao kwa vitendo. Amehimiza ushirikiano baina ya madiwani na watendaji, akiwataka kuondokana na chuki, ubinafsi na kuweka mbele maslahi ya wananchi.

Mkude amesisitiza kuwa uongozi bora wa jiji lenye kasi kubwa ya ukuaji kama Arusha unahitaji umoja, uwajibikaji na utulivu. Amebainisha kuwa misingi hiyo ndiyo itakayowezesha utoaji wa huduma bora kwa wananchi pamoja na utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwa ufanisi na kwa wakati.

Kwa mujibu wa ratiba, Baraza jipya la Jiji la Arusha linatarajiwa kuanza vikao vyake rasmi muda mfupi ujao. Vikao hivyo vitatoa nafasi ya kuanza kupanga ajenda za awali za maendeleo, kupitia mikakati ya usimamizi wa huduma za jamii, pamoja na kuweka mwelekeo wa utekelezaji wa miradi mipya na inayoendelea.

Uzinduzi huu unaiweka Arusha kwenye njia ya awamu mpya ya uongozi unaotazamiwa kuleta mabadiliko chanya, uwazi na kasi katika utendaji wa halmashauri, huku wananchi wakitarajia kuona maboresho zaidi kwenye huduma, miundombinu na usimamizi wa rasilimali za jiji.







 

Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) kwa kushirikiana na Uongozi wa Mkoa wa Tanga na Wilaya ya Mkinga umezindua rasmi na kuendesha zoezi la ulipaji wa fidia kwa wananchi wa kijiji cha Makota, kata ya Mwakijembe  wilayani Mkinga ili kupisha eneo tengefu la Mto Umba kujumuishwa ndani ya mpaka wa Hifadhi ya Taifa Mkomazi leo Desemba 04, 2025.

Akizungumza na wanachi wa eneo hilo Mkuu wa Mkoa wa Tanga Balozi Dkt. Batilda Buriani amesema kuwa hatua hiyo iliyofikiwa kwa pande zote mbili itafungua milango kwa Mkoa wa Tanga kuwa na lango/malango yatakayopokea wageni na wawekezaji nje na ndani ya mipaka ya Tanzania ndani ya Hifadhi ya Taifa Mkomazi kupitia Wilayani Mkinga. 

"Lengo ni kuhakikisha uhifadhi endelevu ndani ya Hifadhi ya Taifa Mkomazi. Eneo hili la Mto Umba litafungua milango ya kuingia katika Hifadhi ya Taifa Mkomazi na wageni wanavyokuja kulingana na ukuaji wa Utalii na Uhifadhi watapata fursa ya kutembelea vivutio vyetu na kuchangia pato la uchumi kwa zaidi ya 6.4% tulizokuwa tukizitengeneza hapo awalii"  amesema Mkuu wa Mkoa wa Tanga. 

Mkuu wa Mkoa aliongeza kuwa hatua hii itasaidia kupunguza na kudhibiti wanyamapori waharibifu hasa Tembo wanaoingilia makazi ya watu na mali zao na kuziharibu hususani msimu wa kilimo na kiangazi. 

"Niwasisitize ndugu zetu wa TANAPA kuendeleza jitihada za kukabiliana na wanyamapori hatarishi na sasa mmekabidhiwa vitendea kazi ikiwemo ndege nyuki zinazowasaidia kuwadhibiti wanyama hao".

Kwa upande wake Naibu  Kamishna wa Uhifadhi na Mkuu wa Kanda ya Kaskazini Steria Ndaga ameeleza kuwa kuna wananchi 115 wanahamishwa katika eneo hilo Tengefu na tathmini imekwisha kamilika na leo watalipwa ili kupisha eneo hilo litumike kwaajili ya shughuli za uhifadhi huku akitaja faida za eneo hilo tengefu kujumuishwa katika eneo la Hifadhi ya Taifa Mkomazi. 

"Eneo hili lina mandhari nzuri ya kuvutia watalii wa aina mbalimbali ikihusisha mimea, ndege na wanyamapori na tafiti mbalimbali zimefanyika na baadae kupitia serikali michakato mingi imefanyika ikaamua eneo hilo lihifadhiwe kwa faida kubwa za kitaifa" amesema Naibu Kamishna wa Uhifadhi. 

Akimkaribisha Mkuu wa Mkoa Tanga, Mkuu wa Wilaya ya Mkinga Mhe. Gilbert Kilima aliwashukuru wananchi wote na kuwapongeza kwa ushirikiano waliouonesha tangu mwanzo wa mchakato huu hadi mwisho. Amesisitiza kuwa  jukumu la uhifadhi ni la wananchi wote na kila mmoja ni mlinzi wa rasilimali za mataifa ikiwemo maliasili. 

Zoezi hilo la ulipaji fidia limesimamiwa na Shirika la Hifadhi za Taifa TANAPA, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Wilaya, viongozi wa serikali ya kata, kiijiji na kitongoji ili kuhakikisha kila mnufaika anapata fidia yake kama ilivyoratibiwa na wathamini wa zoezi hilo.
















Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limesaini makubaliano ya awali na Kampuni ya United Platform Solution (UPS) kwa ajili ya kuanzisha mfumo wa kidigitali wa ufuatiliaji wa uchafuzi wa mazingira katika miradi yote ya maendeleo nchini.

Hafla hiyo ya kusaini makubaliano hayo imefanyika Disemba 04,2025 katika ukumbi wa mikutano wa Baraza uliopo jijini Dar es Salaam.

Akizungumza katika hafla hiyo kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Bw. Dickson Mjinja ambaye pia ni Mkurugenzi wa Utawala na Fedha, amesema Baraza limefikia hatua hiyo ili kurahisisha masuala mazima ya usimamizi na uhifadhi wa mazingira kwani mfumo huo ukikamilika utarahisisha kubaini viashiria vya uchafuzi wa mazingira na kupata taarifa sahihi na kwa wakati kuhusu hali ya mazingira.

Naye Bw Mamadou Drame kutoka UPS alipozungumza amesema imekuwa azma yao kushirikiana na NEMC katika kuhakikisha uchafuzi wa Mazingira unadhibitiwa kidigitali ili kuyalinda kwa maendeleo endelevu.

Akifafanua namna mfumo huo utakavyotenda kazi, Kaimu Mkurugenzi wa Uzingatiaji na Utekelezaji wa Sheria wa NEMC, Bw. Jamal Baruti amesema kwa sasa utaanza mradi wa majaribio ambapo vifaa maalum vitawekwa katika miradi ya mazingira ikijumuisha miradi iliyopo katika Kanda 13 za NEMC nchi nzima hali itakayoimarisha zaidi usimamizi na Uhifadhi wa mazingira nchini.







 

*Na MASHAKA MHANDO, Tanga

WAKIMBIAJI wapatao 200, wengi wao wakiwa ni vijana, wanatarajiwa *kufukuza upepo* katika uzinduzi wa msimu wa kwanza wa 'Msomera Historical Marathon' utakaofanyika Desemba 13 mwaka huu katika Kijiji cha Msomera, wilayani Handeni, Mkoa wa Tanga.

Mbio hizo zimeanzishwa na Kampuni ya Mawasiliano na Uendelezaji Utamaduni nchini (yenye makao makuu Butiama, Mara) kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Handeni.

 **Kuunga Mkono Uamuzi wa Uhamaji**

Mratibu wa shindano hilo, Mashaka Mgeta, alisema mbio hizo zinakwenda kuwakutanisha vijana na wanariadha wakubwa kutoka maeneo mbalimbali nchini ili kuunga mkono dhamira ya wananchi waliokuwa wakiishi wilayani Ngorongoro, Arusha, kuhamia kwa hiari katika Kijiji cha Msomera na kufanya makazi yao ya kudumu.

Mgeta, ambaye kitaaluma ni Mwandishi wa Habari na anahudumu Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Tanga kama Ofisa Habari wa Mkoa, alisema kitendo cha kuacha eneo la Ngorongoro kuendelea kuhifadhiwa na kuendeleza utalii ni suala linalopaswa kuungwa mkono na kupongezwa.

"Kwetu sisi, baada ya kubaini nia yao nzuri ya kuhama kupisha uhifadhi na utalii kule Ngorongoro, tumeanzisha mbio hizi maalum kwa ajili ya kufanya *utetezi na kuelimisha* hasa makundi ya vijana wetu ili waweze kutambua fursa zinazoweza kupatikana kupitia uhifadhi na utalii," alisema Mgeta.

Aliongeza kuwa vijana lazima watambue fursa zinazopatikana katika maeneo mbalimbali kupitia sekta hizo na hivyo kuwa na jukumu la msingi la *kulinda na kuhifadhi* rasilimali za Taifa.

 *Amani na Fursa Katika Riadha*

Mgeta alisisitiza kuwa mbio hizo zinakwenda kufungua mnyororo wa mahusiano na dhamira ya wananchi kutambua na kuacha kwa hiari yao maeneo ya uhifadhi kwa faida ya utalii na uendelezaji wa rasilimali za Taifa.

"Tunataka vijana wajue, pasipokuwa na **amani na utulivu** katika Taifa letu, hatuwezi kunufaika na fursa hizi zilizopo. Mbio hizi zimebeba ujumbe na agenda ya **kudumisha Amani** ili fursa zilizopo nchini ziweze kuwanufaisha vijana katika nyanja mbalimbali," alifafanua.


*Kanuni na Taratibu za Riadha*

Akizungumzia utekelezaji, Katibu wa Chama Cha Riadha Mkoani Tanga (RT), *Ibrahim Adam*, alisema wazo hilo liliungwa mkono na watasimamia mbio hizo kufanyika kwa kufuata kanuni, taratibu na sheria zinazotawala mchezo wa Riadha duniani.

Alithibitisha kuwa kutakuwa na *mbio ndefu (kilomita 42.2)*, *nusu Marathon (kilomita 21)*, *kilomita 10* na zile za **kujifurahisha (kilomita 5)**.

Adam alisema tayari njia zitakazopitwa na wakimbiaji zimefanyiwa ukaguzi, ikiwemo kujiridhisha na maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya vituo vya maji na *juice*, ili kuhakikisha wakimbiaji wanatengeneza wasifu wao huku wakifurahia maeneo ya kihistoria watakayopita wilayani Handeni hadi kufika Kijiji cha Msomera.


Na Mwandishi wetu, Ngorongoro.

Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) kupitia Idara ya Maendeleo ya Jamii imewawezesha  wakinamama 84 kutoka Kata ya Ganako, wilayani Karatu, kufanya ziara ya mafunzo ndani ya Hifadhi ya Ngorongoro baada ya kupewa mafunzo ya kutengeneza majiko banifu ili kulinda mazingira 

Ziara hiyo ni sehemu ya programu ya elimu kwa vitendo inayolenga kuhamasisha uhifadhi wa mazingira na matumizi ya teknolojia rafiki na kuepuka kukata miti na matumizi ya mkaa kwa jamii inayozunguka hifadhi ya Ngorongoro.

Akizungumza katika ziara hiyo, Afisa Maendeleo ya Jamii wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro, Bi. Lightness Kyambile, amesema hatua hiyo inalenga kuwawezesha wanawake kuwa mabalozi wa uhifadhi katika jamii zao ili kuepuka kukata miti, kuchoma mkaa na kuharibu mazingira.

Akina mama walioshiriki ziara hiyo wametoa shukrani kwa uongozi wa Ngorongoro kwa kuwapa nafasi ya kujifunza kwa vitendo na kuahidi  kuendelea kutoa  elimu hiyo kwa wanawake wengine katika vijiji vyao.

Ziara hiyo ya mafunzo  imeandaliwa  kwa kuwashirikisha Ganako Youth, ambao wamekuwa mstari wa mbele kutoa elimu ya utunzaji wa mazingira na kuhamasisha matumizi ya nishati mbadala.






 

Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mussa Azzan Zungu, amekutana na kufanya mazungumzo na baadhi ya Mabalozi wa Nchi Wanachama wa Umoja wa Ulaya wakiongozwa na Balozi wa Umoja wa Ulaya (EU), Mhe. Christine Grau walipomtembelea leo tarehe 4 Desemba, 2025 katika Ofisi Ndogo za Bunge Jijini Dar es Salaam.

Pamoja na mambo mengine, walizungumza kuhusu kuimarisha ushirikiano kati ya Tanzania na Nchi Wanachama wa Umoja wa Ulaya, ikiwa ni pamoja na kuimarisha diplomasia ya kibunge (Parliamentary Diplomacy).

Kikao hicho kimehudhuria na Mabalozi wanaowakilisha nchi zao nchini Tanzania ambao ni Balozi wa Finland, Balozi wa Hispania, Balozi wa Italia, Balozi wa Ubelgiji na Balozi wa Ujerumani.






Top News