• Tanzania, Rwanda na Uganda zakubaliana kusaini hati ya makubaliano ya ujenzi wa Kufua Umeme Nsongezi wa 39MW
Mkutano wa 17 wa Baraza la Mawaziri la Kisekta la Nishati, Petroli na Madini la Jumuiya ya Afrika Mashariki umeipongeza Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kukamilisha maandalizi ya Kongamano na Maonesho ya 11 ya Petroli ya Jumuiya ya Afrika Mashariki yatakayofanyika tarehe 5 hadi 7 Machi 2025 jijini Dar es Salaam.
Pongezi hizo zimetolewa kwenye mkutano wa Baraza hilo uliofanyika katika Makao Makuu ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) jijini Arusha.
Uenyeji wa Tanzania katika Kongamano hilo unatokana na Maamuzi ya Mkutano wa 16 wa Baraza la Mawaziri la Kisekta la Nishati uliofanyika Februari 14, 2024 ambao uliamua Tanzania kuwa Mwenyeji wa Kongamano na maonesho hayo.
Kongamano na Maonesho hayo ni mkakati unaolenga kutangaza fursa zilizopo katika nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki kuhusu rasilimali za mafuta na gesi asilia na kuielezea jiolojia ya ukanda wa Afrika Mashariki ili kuvutia uwekezaji, kuendelezaji wa miundombinu, udhibiti wa uharibifu wa mazingira, usimamizi wa taarifa za mafuta na gesi asilia.
Pia linalenga kutangaza maeneo mapya ya utafutaji na kutangaza maendeleo yaliyopatikana katika sekta ya nishati katika ukanda.
Malengo mengine ni kubadilishana uzoefu kuhusu sera, sheria, kanuni na utaalamu unaotumika kwenye sekta ya nishati, kuhamasisha uwekezaji, utafutaji, uzalishaji na uendelezaji wa mafuta na gesi asilia. Vilevile Kongamano hilo linatoa fursa ya kutangaza vivutio vya utalii vilivyopo nchini na katika ukanda wa Afrika Mashariki.
Kongamano na maonesho hayo yanatoa fursa adhimu kwa Tanzania kutangaza fursa za uwekezaji katika sekta ya Nishati hususan katika sekta ndogo ya mafuta na gesi na hivyo kuongeza wigo wa kupata wawekezaji kwenye sekta hiyo.
Mbali na hayo, Mkutano 17 wa Baraza la Mawaziri la Kisekta la Nishati, Petroli na Madini la EAC limepokea na kujadili taarifa ya utekelezaji wa miradi na programu mbalimbali katika sekta ya nishati, petroli na madini ikiwemo Mradi wa Kufua Umeme wa Nsongezi wenye Megawati 39 kwa kutumia maporomoko ya maji ya Mto Kagera utakaotelezwa kwa pamoja baina ya Tanzania, Rwanda na Uganda.
Ujumbe wa Tanzania katika Mkutano huo wa 17 wa Baraza la Mawaziri la Kisekta la Nishati, Petroli na Madini uliongozwa na Waziri wa Madini Mhe. Antony Mavunde (Mb.), Naibu Waziri wa Nishati Mhe. Judith Kapinga (Mb.), Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Uchumi wa Buluu na Uvuvi- Zanzibar Bw. Zahor Alharousy na Viongozi wengine waandamizi wa Serikali.
Mwanamuziki nyota wa Bongo Flava, Omary Ally Mwanga, anayefahamika kwa jina la kisanii Marioo, ametambulishwa rasmi kama Balozi wa Bahati Nasibu ya Taifa ya Tanzania. Ushirikiano huu wa kimkakati unaleta matumaini, burudani, na fursa zinazoweza kubadilisha maisha ya Watanzania.
Huku Bahati Nasibu ya Taifa ikikaribia kuzinduliwa rasmi, Kampuni ya ITHUBA, ambayeni mwendeshaji rasmi aliyepewa dhamana ya miaka nane, inaleta enzi mpya ya ushindi ambapo kuamini katika uwezekano wa kitu kunageuza ndoto kuwa uhalisia.
Katika kiini cha bahati nasibu hii ni kauli mbiu yenye nguvu: "Amini. Cheza. Ushinde."
Huu sio msemo wa kawaida—bali ni mwamko wa kuhamasisha Watanzania kuota ndoto kubwa, kuthubutu, na kuchukua hatua za kuyafikia mafanikio.
Akizungumzia jukumu lake jipya kama balozi wa Bahati Nasibu ya Taifa, Marioo hakuweza kuficha furaha yake:
"Nina furaha kubwa kutangaza kuwa mimi sasa ni balozi rasmi wa Bahati Nasibu ya Taifa! Huu ni wakati mkubwa—sio tu kwangu kama msanii, bali kwa kila Mtanzania anayethubutu kuota ndoto kubwa. Bahati Nasibu ipo hapa kufungua milango, kutengeneza washindi, na kuinua jamii—nami najivunia kuwa sehemu ya safari hii!"
Ushirikiano huu unamaanisha kwamba ushindi si ndoto tena—bali ni uhalisia unaosubiri kutokea!
Mkurugenzi kutoka ITHUBA Tanzania, Kelvin Koka, alisisitiza kuwa ushawishi wa Marioo unamfanya kuwa kiungo bora kati ya burudani na michezo ya kubahatisha.
"Marioo ni zaidi ya msanii—yeye ni alama ya kizazi kipya cha Watanzania wanaothubutu kuamini katika ndoto zao. Nguvu yake, uhalisia wake, na uhusiano wake wa karibu na mashabiki wake vinamfanya kuwa balozi sahihi wa Bahati Nasibu ya Taifa. Kupitia yeye, tutahamasisha Watanzania wengi zaidi kushiriki kwenye michezo ya bahati nasibu ambayo ni ya haki, ya kusisimua, na yenye uwezo wa kubadilisha maisha," alisema Koka.
Lakini Bahati Nasibu ya Taifa haihusiani tu na ushindi binafsi—ni chombo cha maendeleo kinachowekeza katika miradi ya michezo ili kuinua vipaji na kusaidia jamii.
"Tumejidhatiti katika uwazi, ubunifu, na michezo inayowajibika. Kila tiketi inayouzwa inachangia maendeleo ya taifa, kuhakikisha kuwa washindi si watu binafsi pekee bali ni Watanzania wote kwa ujumla," aliongeza Koka.
Ushirikiano wa Marioo unazinduliwa kwa kampeni kubwa za kitaifa, matukio ya kusisimua, na jackpots za kiwango cha juu ambazo zitawageuza mashabiki wake kuwa washindi.
"Mengi mazuri yanakuja! Kuna jackpots kubwa, matukio makubwa, na fursa kwa mashabiki wangu kushinda kama hawajawahi kushinda kabla. Hii ni mwanzo tu—Tanzania, jiandaeni!" Marioo alidokeza.
Muda wa kusubiri umekwisha. ITHUBA Tanzania iko tayari kuandika historia—ikibadilisha kila siku ya kawaida kuwa siku ya ushindi kwa kila Mtanzania!
Kwa kutumia hashtag rasmi #BahatiNasibuYaTaifa na #Inakuja, Bahati Nasibu ya Taifa inalenga kuongeza ushiriki wa kidijitali na kuwahamasisha Watanzania kote nchini kushiriki.

NA DENIS MLOWE IRINGA
ZAIDI ya bilioni 18 zimetengwa kupitia mradi wa Uboreshaji Miji (TACTIC) kwa ajili ya ujenzi wa soko la kisasa katika kata ya Kihesa na ujenzi wa barabara ya Mkimbizi Mtwivila kwa kiwango cha Lami kupitia bajeti ya mwaka wa fedha 2025/2026.
Hayo yamezungumzwa na Mstahiki Meya wa Halmashauri ya Manispaa ya Iringa Ibrahim ngwada wakati wa Kikao cha Baraza la madiwani kilichokaa hivi karibuni wakati wa Kupitisha Bajeti ya mwaka wa fedha 2025/2026 ya halmashauri hiyo.
Meya Ngwada alisema kuwa katika kuboresha mji wa Iringa watakamilisha miradi mbalimbali likiwemo soko la Kihesa ambalo litakuwa kubwa kuliko soko la kisasa la Mlandege.
Alisema kuwa soko lililopo sasa la Kihesa litabomolewa na kujengwa soko la kisasa ili kukidhi utoaji wa huduma bora kwa wananchi mkoani hapa.
Alisema kuwa hadi sasa halmashauri imeshatekeleza miradi mbalimbali 18 ikiwemo kituo cha afya Mkimbizi ambacho kimeshaanza kufanya kazi, Kituo cha Afya Mkwawa kinaendelea na kazi na uwekezaji shilingi bilioni 3.5 katika hospitali ya Flerimo.
Aliongeza kuwa wamekamilisha mradi mingine kama Wodi ya watoto, karakana ya madawa, wodi za baba na mama, kituo cha afya Isiikalilo, ujenzi kituo cha Afya kata ya Kitwiru.
"* Kwa upande wa Afya hakika mama Samia katupendelea sana kwani vituo na zahanati zimejengwa kusaidia wananchi tunashukuru sana rais wetu kwa kufanikisha yote hayo ndani ya muda mfupi" Alisema
Alisema kuwa elimu miradi mbalimbali imejengwa ikiwemo ujenzi wa mabwenj, shule bora ya kisasa ya eneo la Uyole, Nduli na Kitwiru.
Meya alisema kwa upande wa barabara zitajengwa kwa kiwango cha lami za km5.11 katika kata ya Mtwivila na Mkimbizi ambapo tangazo limeshatoka la ujenzi la kutafuta wakandarasi.
Aidha halmashauri ya Manispaa ya Iringa itajenga jengo la ghorofa moja kwa ajili ya ofisi ya mkandarasi, ujenzi wa daraja kata ya Kitwiru litakalounganisha na kata ya Isakalilo ikiwa ni moja ya ahadi ya rais Samia aliyotoa kwa wananchi mkoani hapa.
Aliongeza kuwa Manispaa itajenga barabara ya mawe kama mfano kutoka shule ya Kiingereza ya Mapinduzi hadi eneo la Sunset Hotel ikiwa ni kuongeza uboreshaji wa barabara hizo ambapo eneo hilo limetengwa kwa ajili ya ujenzi wa mahotel mbalimbali na kutaka wananchi kujitokeza kununua viwanja.
Katika bajeti hiyo maeneo mengine yatakayofaidika ni barabara ya Kondoa Wihanzi hadi Mwembetogwa na Kijificheni, barabara ya kuelekea ofisi ya mkuu wa wilaya ambapo zitajengwa kwa kiwango cha lami.
"Jumla ya Mitaa 11 kunufaika na barabara za lami na vumbi na mawe, manispaa itaongeza taa za barabarani 10 ikiwemo eneo la Makanyagio na kuelekea ikulu ndogo eneo la Gangilonga." Alisema
Kwa upande wake Kaimu Meneja wa Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini TARULA Mkoa wa Iringa Carol Lunyili alisema kupitia mradi wa kimkakati wa Uboreshaji miji (TACTIC) utaboresha miundombinu hasa ya barabara zilizopo katika kata za Mkimbizi Mtwivila na Kihesa kutokana na changamoto zilizopo.
Naye Diwani wa Kata ya Mtwivila Addo Gwegime amewashukuru TARULA wanazofanya na kuwaomba kuzifanyia kazi baadhi ya barabara zilizopo katika kata hiyo kwa kuwa zimekuwa zikiingizwa kwenye bajeti lakini hakuna utekelezaji.
Watanzania kutoka maeneo mbalimbali ya nchi wamejitokeza kwa wingi kutembelea Hifadhi ya Taifa ya Milima Udzungwa kusherehekea Sikukuu ya Wapendanao, Februari 14. Tukio hilo ni sehemu ya kuhamasisha utalii wa ndani na kuunga mkono juhudi za Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika kukuza sekta ya utalii kupitia kampeni mbalimbali.
Akizungumza kwa niaba ya Kamanda wa Kanda ya Mashariki wakati wa hafla maalum ya kuwapokea wageni hao, Kamishna Msaidizi wa Uhifadhi Kanda ya Mashariki TANAPA, Fredrick Malisa, aliwapongeza Watanzania kwa mwitikio wao mkubwa wa kutembelea vivutio vya utalii nchini, akisema kuwa hatua hiyo ni ya kizalendo na inachangia kukuza uchumi wa taifa kupitia sekta ya utalii.
"Ni jambo la kufurahisha kuona Watanzania wakizidi kutambua thamani ya rasilimali za Nchi yao kwa kujitokeza kwa wingi kutembelea vivutio vya utalii. Hii inaonesha uzalendo na mchango wao katika kukuza sekta hii muhimu," alisema Malisa.
Kwa upande wake, Afisa Muhifadhi Mkuu wa Hifadhi ya Taifa ya Milima Udzungwa, Consepta Siima, akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Hifadhi hiyo, Theodora Bathio, alisema mwitikio huo ni ishara ya ongezeko la uelewa kuhusu umuhimu wa utalii wa ndani na faida zake kwa jamii na Taifa kwa ujumla.
"Tunafarijika kuona Watanzania wakishiriki kwa wingi katika utalii wa ndani, hasa katika siku muhimu kama hii ya Wapendanao. Hii ni ishara kwamba juhudi za serikali na wadau wa utalii za kuhamasisha wananchi kutembelea vivutio vyetu zinaendelea kuzaa matunda," alisema Siima.
Naye, Afisa Uhifadhi wa Hifadhi ya Taifa ya Milima Udzungwa, Ahmed Nassor, alieleza kuwa ujio wa wageni wengi katika Hifadhi hiyo unadhihirisha jinsi vivutio vya ndani vinavyothaminiwa na Wananchi.
"Hifadhi ya Milima Udzungwa ina hazina kubwa ya vivutio vya kipekee kama vile maporomoko ya maji ya Sanje, misitu ya mvua yenye viumbe wa kipekee, na njia za kupanda milima zinazotoa mandhari nzuri kwa wapenda mazingira. Tumejipanga kuhakikisha wageni wetu wanapata huduma bora na uzoefu wa kipekee," alisema Nassor.
Kwa upande wa wageni waliotembelea Hifadhi hiyo, Elia Wandwi, mmoja wa watalii wa ndani, alieleza kufurahishwa na uzoefu wake wa kwanza wa kulala kwenye mahema ndani ya Hifadhi, huku akifurahia mazingira ya asili na huduma zilizotolewa.
"Maandalizi na mapokezi yamekuwa mazuri sana. Tumefurahia mandhari ya kuvutia, burudani, na hata vyakula vya asili vinavyoakisi utamaduni wa eneo hili. Ni uzoefu wa kipekee ambao nitaukumbuka kwa muda mrefu," alisema Wandwi.
Utalii wa ndani umeendelea kushamiri Nchini Tanzania kutokana na juhudi za Serikali na wadau mbalimbali wa sekta hiyo. Kampeni kama Royal Tour zimechochea hamasa kubwa kwa Wananchi kujivunia na kutembelea vivutio vyao vya asili, hali inayochangia si tu maendeleo ya sekta ya utalii, bali pia uchumi wa Taifa kwa ujumla.
.jpeg)









