Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akishiriki Mkutano wa Baraza la Amani na Usalama la Umoja wa Afrika (AUPSC) pamoja na viongozi kutoka nchi mbalimbali katika Makao Makuu wa Umoja wa Afrika (AU) Addis Ababa nchini Ethiopia tarehe 14 Februari, 2025.














MKUU wa Mkoa wa Singida, Halima Dendego ameipongeza Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) mkoa wa Singida kwa kupata hati safi “Clean Sheet” ya kukusanya zaidi ya asilimia 100 ya lengo la makusanyo kwa miezi saba mfululizo kuanzia Julai 2024 hadi Januari, 2025

Amesema, mkoa wa Singida umejipanga kuendeleza mafanikio hayo na kuchangia zaidi katika pato la serikali.

Dendego ameyasema hayo alipokutana na maofisa wa TRA kutoka makao makuu ambao wapo mkoani humo kwa ajili ya kutoa elimu ya kodi kwa wadau mbalimbali pamoja na kuwatembelea wafanyabiashara katika maduka yao “Mlango kwa Mlango” kwa lengo la kuwapa elimu ya kodi, kuwasikiliza na kutatua changamoto za kikodi zinazowakabili.

“Niwapongeze na nafurahi mkoa wa Singida kupata “clean sheet”, niaamini kwa ushirikiano tulionao na TRA tutaendelea kupata mafanikio, kwa kweli tumejipanga kuchangia zaidi pato la serikali kwa maendeleo ya nchi yetu kwa kuwa tunawapa elimu walipakodi na wanalipa bila shuruti” amesema Dendego.

Naye Meneja wa Elimu kwa Mlipakodi kutoka TRA, CPA Paul Walalaze amemshukuru Mkuu wa Mkoa wa Singida na kuahidi kuendelea kutoa elimu kwa wadau na wafanyabiashara wa makundi mbalimbali ili kuhakikisha kwamba walipakodi wanaelewa wajibu wao wa kulipakodi kwa mujibu wa sheria pamoja na kuwasaidia namna ya kutumia mifumo ya TRA inayorahisisha ulipaji kodi kwa hiari na kwa wakati.

“TRA itaendelea kuwaelimisha walipakodi na kuwafikia wafanyabiashara na wadau mbalimbali na kuhakikisha kuwa mkoa unaendelea kufanya vizuri katika kukusanya, na tutaendelea kuwaelimisha na kuwapa taarifa muhimu walipakodi wetu ili waweze kulipakodi kwa hiari na kwa wakati”, amesema Walalaze.

 

 MKUU wa Wilaya ya Nachingwea mkoani Lindi Mhe. Mohamed Moyo amewataka wafanyabiashara kuacha tabia ya kupanga bei mbili moja ya risiti na nyingine ya bila risiti jambo ambalo ni kinyume cha sheria. 

Mhe. Moyo amesema hayo leo tarehe 14.02.2025 ofisini kwake alipotembelewa na timu ya maofisa kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) waliofika kujitambulisha kabla ya kuanza zoezi la kutoa elimu ya kodi mlango kwa mlango kwa wafanyabiashara wa Nachingwea mjini.

"Ninawasihi wafanyabiashara kuacha mara moja tabia ya kuuza bidhaa moja kwa bei mbili yaani anayedai risiti anauziwa kwa bei ya juu na asiyedai risiti anauziwa kwa bei ya chini, mtindo huu ni siyo mzuri na unashusha maendeleo ya nchi yetu."  

Mhe. Moyo ameongeza kuwa, maendeleo yanayoonekana katika jamii kama vile barabara, ujenzi wa shule na miundo mbinu mbalimbali ni matokeo ya kodi inayolipwa na wafanyabiashara pamoja na wananchi kwa ujumla  na amesisitiza kwamba, hakuna taifa linaloweza kuendelea na kujitegemea bila ya wanachi wake kulipa kodi.







Na. Josephine Majura, WF - Dodoma


Bunge limepitisha nyongeza ya mapato na matumizi ya jumla ya shilingi bilioni 945.7 kwa ajili ya kuongeza kwenye Bajeti ya Serikali ya mwaka 2024/25 kutoka shilingi trilioni 49.346 iliyoidhinishwa awali hadi shilingi trilioni 50.291.

Nyongeza hiyo imewasilishwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb), ambaye ameeleza kuwa fedha hizo zitakazotekeleza shughuli za sekta za elimu, afya utalii na program mbalimbali za kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabia ya nchi, zimepatikana kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) na Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF).

Alisema shilingi bilioni 325.9 zimetengewa Wizara ya Fedha, kwa ajili ya matumizi ya kitaifa, kugharamia malipo ya madeni ya watumishi, wakandarasi na wazabuni wa ndani pamoja na ujenzi wa miundombinu ya Serikali katika Mji wa Serikali Mtumba.

Mhe. Nchemba aliongeza kuwa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imetengewa shilingi bilioni 131.4 kwa ajili ya kugharamia mahitaji ya Mtaala mpya wa sekta ya elimu ikiwemo ujenzi wa shule za sekondari za amali, upatikanaji wa vifaa na walimu.

“Fedha hizo zitagharamia ukamilishaji wa ujenzi wa vyuo vya VETA, ujenzi wa maktaba ya Chuo Kishiriki cha Elimu Mkwawa (MUCE), ujenzi wa miundombinu ya Chuo cha Nelson Mandela-Arusha, ujenzi wa majengo ya Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima pamoja na ujenzi wa Jengo la Maktaba Mwanza”, alibainisha Mhe. Dkt. Nchemba.

Aliongeza kuwa Wizara ya Afya imeongezewa shilingi bilioni 53.7 kwa ajili ya kugharamia dawa, vifaa tiba na vitendanishi.

Mhe. Dkt. Nchemba alisema Ofisi ya Rais – TAMISEMI imeongezewa shilingi bilioni 173.7 kwa ajili ya sekta ya elimu, afya na kuiwezesha TARURA kukarabati miundombinu ya barabara na madaraja iliyoathirika na mvua za masika ili iweze kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

Alisema shilingi bilioni 260.7 zimetengwa kwa ajili ya Wizara ya Maliasili na Utalii ili kugharamia uendeshaji na ukarabati wa miundombinu ya barabara katika Hifadhi za Taasisi za Utalii za Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) na Mamlaka ya Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA.)

Aidha, Mhe. Dkt. Nchemba alisema mgawanyo huo umezingatia maono ya Mhe. Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuwa na nguvu kazi yenye ujuzi wa kuhakikisha utekelezaji wa elimu ya amali ni unafanyika kwa vitendo.




Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb), akiwasilisha bungeni nyongeza ya mapato na matumizi ya sh. bilioni 945.7 kwa ajili ya kuongeza Bajeti ya Serikali ya mwaka 2024/2025 kutoka shilingi trilioni 49.346 hadi sh. trilioni 50.291 iliyoidhinishwa awali na Bunge.





Baadhi ya viongozi wa Wizara ya Fedha kutoka kushoto ni Mhasibu Mkuu wa Serikali, CPA, Leonard Mkude, Kamishna wa Idara ya Bajeti, Bw. Meshack Anyingisye na Kamishna wa Idara ya Sera Dkt. Johnson Nyella wakifuatilia wasilisho la Waziri wa Fedha Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba (Mb), kuhusu nyongeza ya mapato na matumizi ya sh. bilioni 945.7 kwa ajili ya kuongeza Bajeti ya Serikali ya mwaka 2024/2025 kutoka shilingi trilioni 49.346 hadi sh. trilioni 50.291 iliyoidhinishwa awali na Bunge.



(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, WF- Dodoma)

Na Jane Edward, Arusha 

Wakuu wa wilaya na Wakurugenzi wametakiwa kusimamia kikamilifu suala la lishe katika maeneo yao ili kuwa na Taifa lenye watu wenye afya bora pamoja na utimamu wa akili.

Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa wilaya ya Karatu Dadi Kolimba kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Arusha Paul Christian Makonda katika kikao cha tathmini ya lishe Mkoa wa Arusha.

Kolimba amesema kuwa agenda ya Mheshiwa Rais ni kuhakikisha kila mtanzania anakuwa na afya njema ili kuweza kusaidia kuwa na Taifa lenye watu waliosalama kiafya .

"Mheshiwa Rais ameingia mkataba na wakuu wa mikoa,wakuu wa wilaya na wakurugenzi ambapo imeenda mpaka kwa watendaji wa kata kwasababu ya usalama wa nchi yetu kuanzia usalama wa mama na mtoto kabla na baada ya kuzaliwa"Alisema

Aidha amewaeleza wadau hao wa lishe kuangalia afua za lishe kila wilaya kuona kama zinatekelezwa ili kuwa na tija.

Kwa upande wake Afisa lishe Mkoa Dotto Mirembe anasema kuwa taarifa ya utekelezaji ya viashiria vinavyosimamiwa na mkataba kwa kipindi cha July hadi Desemba 2024 hadi 2025 ambapo mkoa umeweza kutenga bajeti ya afua za lishe ambapo Mkoa umetenga kiasi cha shilingi Milioni 947 ambapo ni sawa na shilingi 2490.4 kwa kila mtoto.

Dotto amesema tathmini ya lishe kwenye ngazi ya kata Mkoa wa Arusha wanafanya vizuri kwa kuwa mpaka sasa wameweza kuvuka lengo la Taifa katika suala la lishe.

Naye Mganga Mkuu wa Mkoa Dkt Charles Mkombachepa kwa niaba ya Katibu tawala wa Mkoa wa Arusha Mussa Misaile amepongeza Afua za lishe kwa kuendelea kufanya vizuri na kuwataka kutobweteka na kuendelea kushika nafasi nzuri katika masuala ya lishe kimkoa.









Mwisho....


Na Jane Edward,Arusha 

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya umishi wa Umma na Utawala Bora, George Simbachawene ,ameitaka Mamlaka ya Serikali Mtandao e-GA kuendelea kufanya tafiti ili kuleta bunifu kwa mifumo ya Tehama katika kuboresha utendaji kazi na kusaidia kuondoa kero ya upatikanaji wa huduma mbalimbali za serikali kwa wananchi.

Chawene ameyasema hayo wakati wa kufunga Kikao Kazi cha 5 cha Serikali Mtandao e-ga kilichofanyika kwa muda wa siku tatu katika ukumbi wa AICC jijini Arusha na kuhudhuriwa na wadau takribani 1500 wakiwemo Maafisa Masuuli, Wakurugenzi na Wakuu wa Vitengo vya TEHAMA, Maafisa TEHAMA na watumiaji wengine wa mifumo ya TEHAMA kutoka katika Taasisi, Halmashauri na Mashirika mbalimbali ya Umma.

Amesema Serikali imedhamiria kuimarisha na kuongeza matumizi TEHAMA ili kwenda sambamba na maendeleo ya Sayansi na Teknolojia kwa kuwa shughuli nyingi duniani ikiwemo za kiuchumi kwa sasa zinafanyika kwa kutumia TEHAMA.

Simbachawene amesema Serikali imetoa kipaumbele kwenye matumizi ya TEHAMA, hususani katika masuala ya utafiti na ubunifu, ili kuimarisha usalama wa Mtandao wa Mawasiliano na kuongeza watumiaji wa internet.

Alisema Wizara kupitia Mamlaka ya Serikali Mtandao (e-GA), imejipanga kupanua wigo wa upatikanaji wa huduma mtandao kwa umma kidijitali sambamba na kuboresha upatikanaji wa mawasiliano ya simu nchi nzima, ili kuwawezesha Watanzania kupata huduma kwa wakati na kwa gharama kupitia mifumo ya TEHAMA,

Waziri Simbachawene amezitaka taasisi za umma kuchukua hatua za haraka ili kuhakikisha zinatumia fursa ya ongezeko hili kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi kidijitali kupitia simu za mkononi.

Naye Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Ikulu,Mulula Mahendeka amesema Vikao vinavyofanyika vimekuwa na manufaa makubwa katika kukuza na kuendeleza jitihada za Serikali Mtandao, kupitia mawazo mbalimbali yanayotolewa na washiriki wa vikao,

Mahandeka amesema Wizara, itasimamia utekelezaji wa maazimio yote yaliyofikiwa kwenye kikao hiki kwa wakati, ikiwa ni kwa Wizara yenyewe, e-GA au taasisi nyingine ya umma inayohusika.

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Serikali Mtandao, Benedict Ndomba aliwashukuru washiriki wote kwa umakini, utulivu na usikivu walioonyesha wakati wote wa kikao, hali ambayo imechangia kupata mawazö bora wakati wa majadiliano.

Alisema mawazo yaliyotolewa ni chachu katika maendeleo ya Serikali Mtandao, na Mamlaka itayafanyia kazi maoni na mapendekezo yote yaliyotolewa kwa kuwa na jitihada za Serikali Mtandao zenye tija zaidi.

Ndomba alisema mawazo jumuishi katika utekelezaji wa jitihada za Serikali Mtandao ni chachu ya kuongeza ufanisi katika utendaji kazi na upatikanaji wa huduma bora kwa wananchi kidijitali, ili kuwezesha upatikanaji wa huduma hizo kwa urahisi, haraka na kwa gharama nafuu,





Mwisho

Serikali za Tanzania na Algeria zimekubaliana kukuza diplomasia ya uchumi kwa kutumia fursa muhimu za kiuchumi zinazopatikana katika nchi hizo mbili ili kujenga ustawi wa watu wake.

Hayo yamejiri wakati Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb.) alipokutana kwa mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje na Diaspora wa Algeria, Mhe. Ahmed Attaf pembezoni mwa Kikao cha 46 cha Baraza la Mawaziri la Umoja wa Afrika kilichofanyika tarehe 12 na 13 Februari, 2025 Addis Ababa, Ethiopia.

Viongozi hao wamejadili juu ya umuhimu wa maandalizi ya Mkutano wa Tume ya Pamoja ya Kudumu ya Ushirikiano (JPC) kati ya Tanzania na Algeria ambapo mara ya mwisho mkutano huo ulifanyika mwaka 2023 jijini Algiers, Algeria. Mkutano ujao ulikubaliwa kufanyika mwaka 2025 nchini Tanzania hivyo, wamekubaliana kuitisha mkutano mwingine mapema ili kuendana na makubaliano ya kuanzishwa kwa tume hiyo yanaoelekeza kuitishwa kwa mkutano huo  kila baada ya miaka miwili ili kuruhusu ufuatiliaji wa utekelezaji katika maeneo ya ushirikiano yaliyokubaliwa.

Pia wamejadili kuimarisha ushirikiano katika sekta ya elimu ambapo, Mhe. Attaf ameahidi kuwa Algeria itaendelea kutoa fursa za ufadhili wa mafunzo ya muda mrefu na mfupi kwa lengo la kujenga uwezo na uzoefu katika masuala mbalimbali ya kitaaluma na kitaalamu.

Vilevile wamesisitiza umuhimu wa kukuza ushirikiano katika sekta ya biashara, nishati na kwenye masuala ya ulinzi, usalama. Pia, uwekezaji katika uzalishaji wa mbolea itakayotosheleza mahitaji halisi ya wakulima nchini Tanzania na kuwezesha kuyafikia malengo ya Mradi wa Jenga Kesho iliyo Bora (BBT) ya kuongeza ajira kwa vijana na kufanya kilimo biashara.

Ushirikiano katika majukwaa ya kikanda na kimataifa ni miongoni mwa masuala yaliyopewa msisitizo ili kuhakikisha nchi hizo mbili  zinasimama imara katika kuunga mkono masuala ya kimkakati na yenye maslahi kwa pande zote katika majukwaa ya kikanda na kimataifa.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb.) akizungumza na Waziri wa Mambo ya Nje na Diaspora wa Algeria, Mhe. Ahmed Attaf pembezoni mwa Kikao cha 46 cha Baraza la Mawaziri la Umoja wa Afrika kilichofanyika tarehe 12 na 13 Februari, 2025 Addis Ababa, Ethiopia.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwasili katika uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Bole, Addis Ababa nchini Ethiopia tarehe 14 Februari, 2025 kwa ajili ya kushiriki Mkutano wa kawaida wa 38 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika (AU). Pamoja na mambo mengine pia Mhe. Rais Dkt. Samia atashiriki mkutano wa Baraza la Amani na Usalama la Umoja wa Afrika























 


Top News