Farida Mangube, Morogoro
Utafiti uliofanywa na Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kupitia mradi wa Kilimo, Chakula na Lishe (FoodLand) umebaini kuwa wakazi wengi wa vijijini hawatumii mayai wala maziwa katika lishe yao, licha ya kufuga kuku, ng’ombe, na mbuzi.
Profesa Susan Nchimbi, mmoja wa watafiti wa mradi huo, alitangaza matokeo ya utafiti huo alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari, akieleza kuwa utafiti ulifanyika katika Wilaya za Kilombero na Mvomero, hasa katika kijiji cha Kinda.
Amesema Utafiti huo ulifanywa kwa njia mbalimbali, ikiwemo madodoso, na umebaini kuwa wananchi wengi wanauza mayai kwa ajili ya kipato badala ya kuyatumia kwa lishe.
Zaidi ya hayo, imegundulika kuwa wananchi wa vijijini hawanywi maziwa kwa sababu wengi hawafugi ng’ombe au mbuzi wa maziwa. Utafiti huu pia umechunguza mbegu bora za maharage zenye madini muhimu, mbinu za ufugaji wa samaki, na uhifadhi wa mazao kama maparachichi, huku ukilenga pia kuboresha elimu ya lishe kwa jamii.
Alisema kuwa katika utafiti walioufanya katika kijiji cha Kinda walibaini kuwa wananchi wa kijiji hicho wanalima Kwa wingi maharage hivyo kupitia utafiti huo wameweza kuja na aina nne za mbegu za maharage ambazo zimeongezewa madini ya chuma na zinki.
Alitaja aina za mbegu hizo maharage ni PIC 130, Nuha 629, Nuha 660 na Mashamba na tayari aina hizi zote zipo kwenye hatua mbalimbali za kufanyiwa majaribio kwenye Mamlaka mbalimbali ikiwemo TOSCI," amesema Prof. Nchimbi.
Profesa Nchimbi alisema utafiti ulilenga pia kwenye ufugaji wa samaki Kwa kuangalia chakula bora cha samaki wa kufungwa lakini pia namna bora ya kuhifadhi mazao hasa matunda mbalimbali yakiwemo maparachichi.
Awali akitoa taarifa ya utafiti huo mmoja wa washiriki wa utafiti huo Prof. Dismas Mwaseba alisema utafiti huo ilianza mwaka 2020 na unafanywa kwenye nchi sita ambazo ni Morocco, Tunisia, Ethiopia, Kenya, Uganda na Tanzania ambapo Kwa Tanzania utafiti huo umefanyika katika mkoa wa Morogoro wilaya ya Kilombero na Mvomero lakini pia katika mkoa wa Dar es Salaam.
Profesa Mwaseba alisema mradi huo umelenga kwenye masuala ya kilimo, elimu, afya na lishe ambapo kwenye upande wa elimu wamebaini kuwa vijana wengi wa kwenye kijiji cha Kinda hawajui kusoma hali ambayo inawafanya washindwe kusoma vipeperushi na majarida mbalimbali yanayoeleza masuala ya lishe na hivyo kujikuta wakishindwa kuzingatia masuala ya lishe.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana na Wenye Ulemavu, Mhe. Ridhiwani Kikwete leo Machi 27, 2025 amezindua Bodi mpya ya Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) na kuagiza Bodi hiyo kusimamia uwekezaji wa Mfuko wenye tija, kusimamia mipango ya Mfuko na kusimamia maadili.
Akizungumza katika hafla hiyo ya uzinduzi wa Bodi, Mhe. Waziri ameelekeza Bodi hiyo kusimamia Sera, Sheria, Kanuni, kuzingatia miongozo mbalimbali inayotolewa na Serikali pamoja na kusimamia misingi ya uwajibikaji, uadilifu, ubunifu na ushirikiano katika kazi.
"Misingi hii ni muhimu kwa sababu inahakikisha PSSSF inafanya kazi kwa ufanisi, usawa na haki, kuepuka rushwa kwa watumishi na viongozi katika kuhakikisha Mfuko unakua endelevu na kukuza uhimilivu wake," alisema Mhe. Kikwete.
Naye Mwenyekiti wa Bodi hiyo, Bi. Mary Mapunjo ameshukuru kwa uteuzi wa wajumbe wa Bodi ambapo amesema kuwa uteuzi huo umezingatia taaluma mbalimbali ambazo zitawezesha ustawi wa Mfuko na kuupongeza utendaji kazi wa PSSSF.
"Wajumbe wa Bodi hii uteuzi wake umezingatia taaluma zote muhimu, kumekua na mchanganyiko mzuri tunaamini kazi itatendwa vizuri," alisema Bi. Mapunjo.
Aidha amesema kuwa Bodi mpya imepokea maelekezo yote aliyotoa na kuahidi kuwa wamejiwekea mikakati ya kutenda kazi kwa kasi ya kukimbia kuendelea pale ambapo Bodi iliyopita ilipoishia.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa PSSSF, Abdul-Razaq Badru alisema Mfuko unaahidi kufanya kazi kwa ushirikiano mkubwa na kuongeza kuwa Mfuko uko kwenye uelekeo mzuri, vitendea kazi na rasilimali watu ya kutosha.
Farida Mangube, Morogoro
Utafiti uliofanywa na Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kupitia mradi wa Kilimo, Chakula na Lishe (FoodLand) umebaini kuwa wakazi wengi wa vijijini hawatumii mayai wala maziwa katika lishe yao, licha ya kufuga kuku, ng’ombe, na mbuzi.
Profesa Susan Nchimbi, mmoja wa watafiti wa mradi huo, alitangaza matokeo ya utafiti huo alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari, akieleza kuwa utafiti ulifanyika katika Wilaya za Kilombero na Mvomero, hasa katika kijiji cha Kinda.
Amesema Utafiti huo ulifanywa kwa njia mbalimbali, ikiwemo madodoso, na umebaini kuwa wananchi wengi wanauza mayai kwa ajili ya kipato badala ya kuyatumia kwa lishe.
Zaidi ya hayo, imegundulika kuwa wananchi wa vijijini hawanywi maziwa kwa sababu wengi hawafugi ng’ombe au mbuzi wa maziwa. Utafiti huu pia umechunguza mbegu bora za maharage zenye madini muhimu, mbinu za ufugaji wa samaki, na uhifadhi wa mazao kama maparachichi, huku ukilenga pia kuboresha elimu ya lishe kwa jamii.
Alisema kuwa katika utafiti walioufanya katika kijiji cha Kinda walibaini kuwa wananchi wa kijiji hicho wanalima Kwa wingi maharage hivyo kupitia utafiti huo wameweza kuja na aina nne za mbegu za maharage ambazo zimeongezewa madini ya chuma na zinki.
Alitaja aina za mbegu hizo maharage ni PIC 130, Nuha 629, Nuha 660 na Mashamba na tayari aina hizi zote zipo kwenye hatua mbalimbali za kufanyiwa majaribio kwenye Mamlaka mbalimbali ikiwemo TOSCI," amesema Prof. Nchimbi.
Profesa Nchimbi alisema utafiti ulilenga pia kwenye ufugaji wa samaki Kwa kuangalia chakula bora cha samaki wa kufungwa lakini pia namna bora ya kuhifadhi mazao hasa matunda mbalimbali yakiwemo maparachichi.
Awali akitoa taarifa ya utafiti huo mmoja wa washiriki wa utafiti huo Prof. Dismas Mwaseba alisema utafiti huo ilianza mwaka 2020 na unafanywa kwenye nchi sita ambazo ni Morocco, Tunisia, Ethiopia, Kenya, Uganda na Tanzania ambapo Kwa Tanzania utafiti huo umefanyika katika mkoa wa Morogoro wilaya ya Kilombero na Mvomero lakini pia katika mkoa wa Dar es Salaam.
Profesa Mwaseba alisema mradi huo umelenga kwenye masuala ya kilimo, elimu, afya na lishe ambapo kwenye upande wa elimu wamebaini kuwa vijana wengi wa kwenye kijiji cha Kinda hawajui kusoma hali ambayo inawafanya washindwe kusoma vipeperushi na majarida mbalimbali yanayoeleza masuala ya lishe na hivyo kujikuta wakishindwa kuzingatia masuala ya lishe.
Mwisho.
Mwisho.
NA WILLIUM PAUL, MOSHI.
MBUNGE wa viti maalum kupitia mkoa wa Kilimanjaro, Zuena Bushiri ameendelea kusapoti Umoja wa Wanawake wa chama cha Mapinduzi(UWT) mkoa wa Kilimanjaro ambapo amekabidhi mabati 50 kwa ajili ya kuezekea nyumba ya Katibu wa mkoa wa UWT.
Hatua hiyo ni kuhakikisha Mtumishi huyo anaishi katika nyumba ambayo itakuwa ni mali ya UWT ambapo mabati hayo amemkabidhi Mwenyekiti wa UWT mkoa wa Kilimanjaro, Elizabeth Minde pamoja na Katibu wake, Erimina Mushongi.
Akikabidhi mabati hayo, Mbunge huyo alisema kuwa, anaunga mkono zilizoanzishwa na UWT kuhakikisha watumishi wake ambao ni Makatibu wa UWT wilaya na mkoa wanapata nyumba.
Aliahidi kuendelea kushirikiana na wanachama wa UWT mkoa wa Kilimanjaro kuhakikisha nyumba hiyo inakamilika mapema na Katibu anahamia hapo.
Akitoa shukrani kwa Mbunge huyo, Mwenyekiti wa UWT mkoa wa Kilimanjaro, Wakili Elizabeth Minde alimshuku Zuena kwa jinsi ambavyo amekuwa akijitoa kuisapoti Umoja huo katika mambo mbalimbali.
"Mbunge Zuena ni mbunge wa kuigwa kwani amekuwa mstari wa mbele kujitoa katika maswala yanayohusu Umoja huo pamoja na chama hivyo nimshukuru sana kwa leo kutukabidhi mabati haya 50 na ametuahidi kuendelea kushirikiana na sisi mpaka ujenzi wa nyumba hii utakapokamilika" Alisema Wakili Elizabeth.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea Taarifa ya Mwaka ya Utendaji Kazi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kutoka kwa Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi hiyo Bw. Crispin Chalamila kwenye hafla fupi iliyofanyika Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 27 Machi, 2025.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa mwaka 2023/24 kutoka Bw. Charles Kichere kwenye hafla fupi iliyofanyika Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 27 Machi, 2025.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na viongozi mbalimbali mara baada ya kupokea Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa mwaka 2023/24 pamoja na Taarifa ya Mwaka ya Utendaji Kazi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 27 Machi, 2025.
Viongozi mbalimbali wakiwa kwenye hafla ya kupokea Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa mwaka 2023-2024 pamoja na Taarifa ya Mwaka ya Utendaji Kazi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Ikulu Jijini Dar es Salaam
Na Mwandishi Wetu
MRADI wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP) umefikia hatua muhimu kwa kufanikisha upatikanaji wa sehemu ya kwanza ya ufadhili wa nje, hatua inayoweka msingi madhubuti kwa uwekezaji mkubwa zaidi wa miundombinu katika kanda hii.
Ufadhili huo, uliopatikana kutoka kwa muungano wa taasisi za kifedha, unaonesha imani kubwa katika ufanisi wa mradi huu na uwezo wake wa kuleta mageuzi katika sekta ya nishati ya Afrika Mashariki.
Washirika wa kifedha wanaounga mkono mradi huu ni pamoja na benki mashuhuri za kikanda kama African Export-Import Bank (Afreximbank), The Standard Bank of South Africa Limited, Stanbic Bank Uganda Limited, KCB Bank Uganda, na The Islamic Corporation for the Development of the Private Sector (ICD).
Ahadi hiyo kutoka kwa taasisi hizi za kifedha inaonesha uungwaji mkono mkubwa kwa maono ya EACOP na nafasi yake muhimu katika kufanikisha usafirishaji wa mafuta ya Uganda kwenye soko la kimataifa.
Kukamilika kwa sehemu hiyo ya kwanza ya ufadhili ni hatua muhimu kwa EACOP na wanahisa wake: TotalEnergies (62%), Uganda National Oil Company Limited (UNOC 15%), Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC 15%), na China National Offshore Oil Corporation (CNOOC 8%).
Ushirikiano wao wa pamoja unahakikisha kuwa mradi huu unasonga mbele kama mfumo wa kipekee wa kusafirisha mafuta, ambao utaongeza maendeleo ya kiuchumi kwa Uganda na Tanzania.
Ujenzi wa bomba hilo lenye urefu wa kilomita 1,443, likijumuisha kilomita 296 nchini Uganda na kilomita 1,147 nchini Tanzania, umepiga hatua kubwa. Kufikia machi mwaka 2025, maendeleo ya mradi yamefika asilimia 55,huku kipaumbele kikiwekwa kwenye usalama, uendelevu wa mazingira, na ushirikishwaji wa jamii za wenyeji.
Zaidi ya raia 8,000 kutoka Uganda na Tanzania wameajiriwa katika mradi huu, huku zaidi ya saa 400,000 za mafunzo zikitolewa kwa wafanyakazi ili kuwajengea ujuzi wa msingi.
Hadi sasa, zaidi ya dola milioni 500 za kimarekani zimesambazwa katika uchumi wa ndani kupitia ununuzi wa bidhaa na huduma, jambo linalodhihirisha athari chanya za kiuchumi za mradi huu.
Mradi wa EACOP ukikamilika, bomba hili litakuwa na uwezo wa kusafirisha hadi mapipa 246,000 ya mafuta ghafi kwa siku kutoka Kabaale, wilaya ya Hoima nchini Uganda, hadi kwenye rasi ya Chongoleani, Tanga nchini Tanzania.
Bomba hilo limeundwa kwa teknolojia ya kisasa, likiwa na mfumo wa bomba lenye upana wa inchi 24 lenye insulation na lililozikwa ardhini, vituo sita vya kusukuma mafuta, na vituo viwili vya kupunguza shinikizo. Eneo la usafirishaji wa mafuta baharini lililopo Tanzania litajumuisha mtambo wa umeme wa jua wa 3 MWp, kuonyesha dhamira ya mradi wa kutumia nishati mbadala.
Kwa kuzingatia viwango vya juu vya mazingira na kijamii, mradi wa EACOP umejipanga kufuata miongozo ya Shirika la Fedha la Kimataifa (IFC) na Kanuni za Equator, kuhakikisha utekelezaji wake unazingatia uwajibikaji wa kijamii na uendelevu wa mazingira.
Aidha, mradi huo umeunganishwa na gridi za kitaifa za umeme, ambazo zinategemea nishati ya maji, ili kupunguza athari za kaboni.
Mradi wa EACOP unawakilisha zaidi ya bomba la kusafirisha mafuta; ni alama ya ushirikiano wa kikanda, maendeleo ya kiuchumi, na ustawi wa viwanda.
Uwekezaji katika mafunzo, ajira, na ununuzi wa ndani unahakikisha kuwa jamii zinazopitiwa na bomba hili zinanufaika na fursa za kiuchumi za muda mrefu.
Kwa msaada wa taasisi kuu za kifedha na dhamira ya maendeleo endelevu, EACOP imejizatiti kuwa kichocheo cha mabadiliko ya kiuchumi Afrika Mashariki.
Kadri mradi unavyoendelea kuelekea kukamilika, unaendelea kuthibitisha kuwa miundombinu ya nishati endelevu inaweza kupatikana kwa njia ya ushirikiano, uvumbuzi, na kufuata viwango vya kimataifa.
Kwa msingi madhubuti wa kifedha sasa ukiwa umekamilika, EACOP itachochea ukuaji wa uchumi, kuboresha biashara za kikanda, na kuchangia usalama wa nishati wa Afrika Mashariki kwa miaka ijayo.
NA VICTOR MASANGU,KIBAHA
Serikali ya awamu ya sita kupitia wizara yake ya mifugo na uvuzi imeanza kutekeleza azma yake ya mpango wa kuwasaidia wafugaji ambapo imetoa chanjo dozi 178,000 kwa halmashauri ya wilaya Kibaha na Bagamayo kwa ajili ya mifugo yao ikiwa ni moja ya chanjo zinazotolowe katika kampeni ya kitaifa kwa ajili ya uchanjaji wa mifugo hiyo ambayo lengo lake kubwa ni kuweza kudhibiti na kutokomeza magonjwa ya mifugo hapa nchini.
Hayo yamebainishwa na Mkurugenzi wa Operesheni kutoka kiwanda cha chanjo za wanyama cha Hester Biosciences Afrika Limited ambacho ndio kinatengeneza chanjo hizo Ms. Chistine Sokoine wakati wa halfa ya kukabidhi chanjo katika Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha pamoja na Bagamoyo.
Mkurugenzi huyo amebainisha kwamba wamefanikiwa kutoa chanjo hizo zipatazo dozi 178,000 ambazo ni za aina mbili ikiwemo za Homa ya Mapafu ya Ng’ombe (CBPP) na Sotoka ya Mbuzi na Kondoo (PPR) ambazo zitatumika kuwachanja wanyama hao.
Aidha Mkurugenzi huyo amebainisha kwamba serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Dr. Samia Suluhu Hassan imewapa dhamana kupitia kiwanda hicho ikiwa ni miongoni mwa viwanda vya ndani kuzalisha na kusambaza chanjo hizo katika kampeni ya kitaifa ya kuchanja mifugo dhidi ya magonjwa mbalimbali.
Ameongeza kwamba zoezi la usambazaji wa chanjo hizo limefanyika katika Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha kwa kukabidhi chanjo ya Mapafu ya Ng’ombe (CBPP) dozi zipatazo elfu 47,000 na ya Sotoka ya Mbuzi na Kondoo (PPR) dozi elfu 60,000.
Kadhalika Mkurugenzi huyo ameongeza kuwa kwa upande wa Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo wameweza kukabidhi chanjo aina ya Mapafu ya Ng’ombe (CBPP) dozi zipatazo elfu 36,000 na ya Sotoka ya Mbuzi na Kondoo (PPR) dozi elfu 35,000 ambazo zimemetolewa na serikali ya Jamuhuri wa Muungano wa Tanzania kwa ajili ya kuwasaidia wafugaji kuchanja mifugo yao.
"Chanjo hizi ambazo tumeweza kuzisambaza katika Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha pamoja na Halmashauri ya Bagamoyo jumla ni dozi 178,000 na kwamba utoaji wa chanjo hizi ni moja ya mgao wa chanjo katika kampeni ya kitaifa ambayo ipo chini ya serikali kupitia Wizara yake ya mifugo na uvuvi ili kuwasaidia wafugaji katika kuchanja mifugo yao na kuondokana na kutokomeza magonjwa mbali mbali,"amebainisha Mkurugenzi huyo.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa kiwanda hicho Ndg.Raj Gera amesema kwamba lengo lao kubwa kama wawekezaji ni kuendelea kushirikiana na serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania katika kuhakikisha inawasaidia wafugaji kupata huduma ya uchanjaji wa mifugo yao kwa lengo la kuweza kudhibiti na kutokomeza magonjwa mbali mbali kwa wanyama.
Mkuu wa Idara ya kilimo,mifugo na uvuvi Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha Ms. Evelyne Ngwira wameishukuru sana serikali ya awamu ya sita kwa kuweza kuwapatia msaada wa chanjo kwa ajili ya mifugo mbali mbali ikiwemo, mbuzi, kondoo, ng'ombe, pamoja na mifugo mingine midogo midogo.
Naye Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha Bi. Regina Bieda amemshukuru kwa dhati Rais wa awamu ya sita Dkt, Samia Suluhu Hassan kwa kuweza ktenga fedha nyingi kupitia Wizara ya mifugo na uvuvi ambazo zitakwenda kuwa ni mkombozi mkubwa wa wafugaji katika suala zima la kuwachanja wanyama wao na kuepukana na magonjwa mbali mbali.
Hivi karibuni Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 216 kwa ajili ya utekelezaji wa mpango huo kwa kipindi cha miaka mitano kuanzia mwaka 2024 hadi mwaka 2029 ambapo kiwanda cha Hester Biosciences Afrika Limited ni miongoni mwa viwanda vya ndani ambavyo vimepewa jukumu kwa ajili ya utengeenzaji wa chanjo hizo zinazotumika kwa wanyama wa aina mbalimbali kama mbuzi,kondoo,Ng'ombe na wanyama wengine wadogo wadogo.
FARIDA MANGUBE, MOROGORO
Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba Tanzania (TMDA) imekabidhi dawa, vifaa tiba na vitendanishi vyenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 19 kwa magereza ya mkoa wa Morogoro.
Dawa hizo zimetolewa baada ya msako mkubwa uliofanywa na TMDA Kanda ya Kati katika mikoa ya Dodoma, Iringa, Singida na Morogoro, ambapo ziliondolewa sokoni kwa kutokidhi vigezo vya kanuni ya TMDA ya mwaka 2015.
Akizungumza wakati wa hafla ya makabidhiano, Meneja wa TMDA Kanda ya Kati, Sonia Henry Mkumba, alisema dawa hizo ni salama na bora kwa matumizi ya binadamu na zimekabidhiwa kwa magereza ili zitumike katika vituo vya afya vilivyo chini ya magereza ya mkoa huo.
Mkumba alifafanua kuwa dawa na vifaa tiba hivyo vilipatikana baada ya mamlaka hiyo kufanya ukaguzi na kuondoa dawa zilizouzwa katika maduka yasiyo na vibali vya kutunza na kukuza dawa kwa mujibu wa kanuni za TMDA za mwaka 2015 na marekebisho yake ya mwaka 2018.
Kwa upande wake, Afisa Mnadhimu wa Magereza Mkoa wa Morogoro, ACP Godfrey Boniface Kavishe, aliishukuru TMDA kwa msaada huo, akibainisha kuwa dawa hizo zitakuwa na mchango mkubwa katika utoaji wa huduma za afya kwa jamii ya magereza.
"Dawa hizi zitagawiwa katika vituo 13 vya afya vya magereza mkoani Morogoro, na tunahakikisha kuwa zitatumika ipasavyo kwa mujibu wa miongozo ya afya," alisema ACP Kavishe.
Hatua hii ni sehemu ya jitihada za TMDA kuhakikisha kuwa dawa zinazosambazwa kwa wananchi zinakidhi viwango vya ubora na usalama, sambamba na kudhibiti usambazaji wa dawa zisizo na vibali katika soko la Tanzania.
FARIDA MANGUBE, MOROGORO
Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imeeleza kuwa itaendelea kutoa elimu kwa wafanyabiashara badala ya kutumia nguvu kama vile kufunga maduka kwa wale ambao hawajalipa kodi kwa wakati.
Akizungumza wakati akitoa elimua kwa mlipa kodi kupitia moja ya redio mjini Morogoro, Meneja Msaidizi wa Huduma kwa Mlipakodi wa TRA, Chacha Boaz Gotora, alisema kuwa mamlaka hiyo imejipanga kuhakikisha wafanyabiashara wanapata uelewa mzuri kuhusu sheria za kodi ili kuepusha usumbufu katika biashara zao.
"Tunatilia mkazo utoaji wa elimu kwa walipa kodi ili kuwawezesha kuelewa wajibu wao. Ni muhimu wafanyabiashara kufahamu kwamba kulipa kodi ni jukumu la kila mmoja kwa maendeleo ya taifa," alisema Gotora.
Akifafanua kuhusu mifumo ya kodi, Gotora alieleza kuwa kodi ya mapato kwa wafanyakazi inatozwa kulingana na kiwango cha mshahara.
Mfano wake ni kwamba mfanyakazi anayepokea mshahara wa kuanzia shilingi 200,000 anapaswa kulipa kodi kwa mujibu wa viwango vilivyowekwa na TRA.
Kwa upande wa wafanyabiashara, Gotora alisema kuwa wanagawanyika katika makundi tofauti, ikiwa ni walipakodi binafsi na makampuni. Kila kundi lina taratibu zake za ulipaji kodi, ambapo wafanyabiashara wadogo na wa kati wanatakiwa kujikadiria kodi zao kulingana na mtaji walio nao.
"Ikiwa mfanyabiashara ana mtaji wa shilingi milioni 100, anatakiwa kuzingatia viwango vya kodi vilivyowekwa na TRA," alieleza.
Kwa mujibu wa TRA, mfanyabiashara yeyote mwenye mauzo ya shilingi 700,000 anatakiwa kulipa kodi ya shilingi 250,000 kwa mwaka, huku makampuni yakitakiwa kulipa kodi kulingana na faida wanayopata baada ya gharama za uendeshaji.
Aidha ameendelea kusisitiza kuwa wafanyabiashara na wafanyakazi wanapaswa kuelewa na kuzingatia sheria za kodi ili kuepuka changamoto zinazoweza kujitokeza kutokana na kutofuata taratibu sahihi za ulipaji kodi.
FARIDA MANGUBEM MOROGORO
Zaidi ya vitongoji 16,000 vinatarajiwa kupata umeme ndani ya miaka miwili ijayo, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuhakikisha tatizo la ukosefu wa nishati hiyo linabaki kuwa historia.
Haya yanakuja licha ya kwamba tayari Wakala wa Nishati Vijijini (REA) umekamilisha mradi maalumu wa kusambaza umeme kwenye migodi ya madini, ambapo zaidi ya maeneo 550 yamepatiwa huduma hiyo.
Vilevile, REA imepeleka umeme wa uhakika kwenye vituo 553 vya kusambazia maji safi na salama kwa wananchi kote nchini.
Hayo yameelezwa na Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi wa REA Mhandisi Hassan Saidy, ambaye pia ni Mkurugenzi Mkuu wa wakala huo, wakati wa ufunguzi wa kikao cha sita cha baraza hilo.
Mhandisi Saidy amesema kuwa REA ni taasisi yenye uwezo mkubwa wa kutekeleza na kufanikisha malengo ya serikali kwa manufaa ya taifa. Amebainisha kuwa wakala huo umeendelea kutekeleza miradi mikubwa yenye matokeo chanya kwa Watanzania.
Hadi sasa, REA imefanikisha miradi minne mikubwa, ikiwemo mradi wa kupeleka umeme vijijini awamu ya tatu, ambapo vijiji 5,259 vimepatiwa umeme. Mradi mwingine mkubwa uliofanikishwa ni ule uliohudumia mikoa minane, ambapo maeneo 426 yamenufaika na nishati hiyo.
Aidha, Mhandisi Saidy amesema kuwa miradi mingine inayoendelea kutekelezwa ni pamoja na:
Mradi wa Ujazilizi Awamu ya Pili B, ambapo vitongoji zaidi ya 1,600 vitapatiwa umeme.
Mradi wa Ujazilizi Awamu ya Pili C, utakaonufaisha vitongoji 1,800.
Mradi wa umeme kwa Wilaya ya Lindi, ambapo vitongoji 293 vitapatiwa nishati hiyo.
Mradi Maalumu wa Kila Jimbo, unaolenga kupeleka umeme kwenye vitongoji 15 kwa kila jimbo, sawa na jumla ya vitongoji 3,060 kote nchini.
"Kazi hizi zote zinatekelezwa kwa weledi na ufanisi mkubwa na wafanyakazi wa REA, hivyo kuna kila sababu ya kuwapongeza kwa juhudi zao chini ya mwavuli wa serikali yetu inayoongozwa na mama shupavu," alisema Mhandisi Saidy.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu wa Wizara ya Nishati, Bibi Ziana Mlawa, amewataka wajumbe wa baraza hilo kutumia kikao hicho kujadili masuala yenye tija ili kusaidia taasisi kufikia malengo ya serikali ya kusambaza huduma ya umeme kwa wananchi.
Naye, Mwakilishi wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya (TUGHE) Taifa, Dkt. Elias Mtungilwa, amesema kuwa wajibu mkubwa wa chama hicho ni kusimamia na kulinda haki na maslahi ya wafanyakazi, huku pia wakihakikisha kuwa haki hizo zinapatikana na kulindwa ipasavyo.
Baraza la Wafanyakazi wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), likiongozwa na Mwenyekiti wake, Mhandisi Hassan Saidy, limekutana mjini Morogoro kwa muda wa siku mbili kujadili masuala mbalimbali yanayohusu maendeleo ya taasisi hiyo.
Dar es Salaam, 27 Machi 2025. Bahati Nasibu ya Taifa ya Tanzania leo imesaini ushirikiano na jukwaa bora la huduma za kifedha kwa njia ya simu hapa nchini, Vodacom M-pesa, Ili kurahisisha miamala ya bahati nasibu ya Taifa na kupanua fursa za kibiashara kupitia mfumo wa fedha wa kidijitali.
Kuunganishwa kwa bahati nasibu ya Taifa kwenye jukwaa la M-Pesa, kutawapa watumiaji urahisi wa upatikanaji wa michezo ya bahati nasibu kupitia jukwaa salama.
Kwa kutumia mtandao mpana wa Vodacom wenye zaidi ya watumiaji milioni 26, ushirikiano huu utawezesha urahisi wa ununuzi wa tiketi za michezo ya kubahatisha, kupitia majukwaa ya kidijitali ya Vodacom, ikiwemo huduma za M-pesa kwa njia ya simu, USSD codes na aplikesheni ya M-pesa.
Mkurugenzi wa ITHUBA Tanzania, Kelvin Koka, ameelezea ushirikiano huu kuwa ni hatua kubwa katika sekta ya michezo ya kubahatisha nchini. "Ushirikiano huu na M-Pesa utahakikisha kwamba wachezaji wanashiriki kikamilifu katika michezo ya bahati nasibu, huku ukihamasisha wafanyabishara kuweza kushirikiana nasi kwa kuwa jukwaa letu linazingatia uwazi na mustakabali ujao wa bahati nasibu ya Taifa. Kwa kuwa M-Pesa ni mshirika wetu rasmi wa huduma za kifedha kwa njia ya simu, tutahakikisha kwamba tunazingatia usalama, ufanisi na uhakika wa miamala ya wateja wetu."
Mkuu wa Idara ya wa M-pesa Tanzania, Jacqueline Ikwabe, amebainisha umuhimu wa ushirikiano huu kwa kusema, "M-Pesa imejikita katika kuwezesha uvumbuzi wa kidijitali unaowanufaisha wafanyabiashara na wateja. Kwa kuiunganisha Bahati Nasibu ya Taifa kwenye jukwaa letu, tutahakikisha ushiriki salama, wa haraka na rahisi huku tukifungua fursa zaidi za ushirikiano katika sekta mbalimbali."
Bahati Nasibu ya Taifa inalenga kutumia ushirikiano huu kuongeza uelewa wa huduma zake na kuimarisha uaminifu kabla ya uzinduzi rasmi wa Bahati nasibu ya Taifa. Hatua hii inatarajiwa kuweka msingi wa ushirikiano katika sekta ya michezo ya kubahatisha na fedha nchini Tanzania.
Ujumuishwaji wa jukwaa la Bahati nasibu ya Taifa kwenye majukwaa ya Vodacom Tanzania utarahisisha ununuzi wa tiketi na upatikanaji wa maudhui ya michezo ya kubahatisha kwa Watanzania wengi zaidi hapa nchini. Hatua hii ya kimkakati inatarajiwa kuongeza ushiriki wa umma, kupanua wigo wa huduma na kuhakikisha ushiriki mpana kutoka kwa makundi mbalimbali ya watu.
MWISHO
Kuhusu ITHUBA
ITHUBA ni muendeshaji rasmi wa Bahati Nasibu ya Taifa ya Tanzania, aliyeteuliwa kwa kipindi cha miaka nane kuanzia mwaka 2025. Kama sehemu ya kampuni inayoongoza katika uendeshaji wa bahati nasibu barani Afrika, ITHUBA inaleta utaalamu na ubunifu wa hali ya juu hapa Tanzania, kwa kuhakikisha uzoefu wa michezo ya kubahatisha wa viwango vya kimataifa. Kampuni imejizatiti kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi, kuimarisha ajira, na kusaidia miradi ya michezo na jamii kwa ujumla.