Dar es Salaam

Benki ya NMB imeendelea kuthibitisha uongozi wake katika masuala ya rasilimali watu baada ya kutunukiwa tuzo maalum na Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) kwa kuzingatia kikamilifu kanuni na uwasilishaji wa michango kwa wakati.

Tuzo hiyo ilitolewa wakati wa maadhimisho ya miaka 10 ya WCF yaliyofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam, yakihusisha viongozi wa serikali, wadau wa ajira, waajiri na mifuko ya hifadhi ya jamii kutoka sekta mbalimbali nchini.

Tuzo kwa NMB ilipokelewa kwa niaba ya benki hiyo na Mkuu wa Idara ya Rasilimali Watu, Onesmo Kabeho.

Akizungumza wakati wa maadhimisho hayo, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa (Mb), aliipongeza menejimenti ya WCF kwa utekelezaji mzuri wa majukumu yake kwa kipindi cha miaka 10. Alimpongeza pia Mkurugenzi Mkuu wa WCF, Dkt. John Mduma, kwa kuendelea kuiongoza taasisi hiyo kwa weledi na mafanikio tangu kuanzishwa kwake.

Mhe. Majaliwa alisisitiza kuwa huduma za fidia kwa wafanyakazi si suala la hiari bali ni haki ya msingi inayopaswa kulindwa na kusimamiwa kwa uwajibikaji wa hali ya juu. Aliongeza kuwa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan itaendelea kufanya maboresho ya maslahi ya wafanyakazi ili kuhakikisha haki na usawa mahali pa kazi vinaimarika zaidi.

Kaulimbiu ya mwaka huu, “Miaka 10 ya Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi: Kazi Iendelee,” ilielezwa na Waziri Mkuu kuwa inaakisi mafanikio makubwa yaliyopatikana katika kipindi cha muongo mmoja.

Kupitia tuzo hii, NMB imedhihirisha dhamira yake ya dhati ya kuwa mwajiri anayeongoza kwa kuzingatia haki, ustawi na usalama wa wafanyakazi wake, sambamba na kuchangia maendeleo endelevu ya taifa.








NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

LICHA ya sekta ya bahari kuwa na mchango mkubwa katika kukuza uchumi wa dunia, bado dunia inakabiliwa na upungufu mkubwa wa mabaharia.

Ameyasema hayo Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Wakala wa Meli Tanzania (TASAC), Bw. Mohamed Salum, katika Maonesho ya 49 ya Kimataifa ya Biashara ya Sabasaba, yanayoendelea katika viwanja vya Mwalimu Nyerere barabara ya Kilwa Jijini Dar es Salaam.

Amesema kuna umuhimu wananchi kujikita katika kusoma masomo ya bahari na kupata mafunzo ya kitaalamu ili kujaza pengo lililopo la mabaharia duniani.

“Hadi sasa kuna uhaba mkubwa wa mabaharia duniani, lakini sekta ya bahari ni eneo lenye fursa nyingi, linachangia kwa kiasi kikubwa katika uchumi wa taifa na kimataifa,” amesema Bw. Salum.

Kuhusu ushiriki wa TASAC katika maonesho hayo, alisema kuwa lengo ni kutoa elimu kwa wananchi juu ya fursa zilizopo katika sekta ya bahari pamoja na kujenga uelewa kuhusu kazi na majukumu ya TASAC.

Bw. Salum alibainisha kuwa TASAC ina jukumu la kusimamia masuala yote yanayohusiana na usalama wa meli, mazingira ya baharini, na utekelezaji wa Mkataba wa Usalama wa Meli na Maeneo ya Bandari (ISPS Code).

Aidha, aliongeza kuwa taasisi hiyo inahusika na ukaguzi wa vyombo vya usafiri majini, utoaji wa vibali kwa maeneo yanayofaa kwa ujenzi wa bandari, pamoja na kudhibiti uchafuzi wa mazingira unaotokana na shughuli za usafiri majini.

“TASAC inahakikisha vyombo vya usafiri majini vinakaguliwa mara kwa mara, usalama unazingatiwa bandarini, na mazingira ya bahari yanatunzwa kwa kudhibiti uchafuzi,” aliongeza.

Mwisho, alihimiza vijana kuchangamkia masomo ya ujuzi wa bahari na kujiunga na taasisi zinazotoa mafunzo ya mabaharia ili kujipatia ajira ndani na nje ya nchi.


Wizara ya Katiba na Sheria imeibuka mshindi wa kwanza kati ya wizara zote zilizoshiriki katika Maonesho ya 49 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam maarufu kama Sabasaba, yanayofanyika kwenye viwanja vya Mwalimu Nyerere, Barabara ya Kilwa.

Akizungumza wakati wa ziara yake kwenye maonesho hayo, Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Jumanne Sagini, aliwataka wananchi kutembelea banda la wizara hiyo ili kupata elimu juu ya masuala mbalimbali ya kisheria.

Alieleza kuwa wananchi wameonyesha mwitikio mkubwa na kuridhika na huduma zinazotolewa, hasa msaada wa kisheria na elimu kuhusu Katiba.

“Wananchi wengi wamefika kupata elimu na msaada wa kisheria. Nawapongeza wataalamu wetu pamoja na mawakili waliopo hapa kwa kujitolea kwao kutoa huduma muhimu kwa jamii,” alisema Sagini.

Akiwa kwenye ziara hiyo, Naibu Waziri pia alitembelea Banda la Mahakama na Wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini (RITA), ambapo alishuhudia idadi kubwa ya wananchi wakihudumiwa hususan katika kupata vyeti vya kuzaliwa.

Alikumbusha kuwa huduma kama hizi zinapatikana hadi ngazi ya wilaya hivyo si lazima kusubiri maonesho.

Sagini aliishukuru Serikali ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuboresha miundombinu ya viwanja vya maonesho na kuwezesha taasisi mbalimbali kufikisha huduma karibu zaidi na wananchi.

Kwa upande mwingine, aliangazia umuhimu wa kampeni ya msaada wa kisheria, akisema serikali imeweka kipaumbele kueneza huduma hiyo hadi kwenye halmashauri kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa sheria.

Pia, alisisitiza umuhimu wa elimu ya sheria katika masuala kama ardhi na ndoa, ambapo migogoro mingi hutokana na ukosefu wa uelewa wa kisheria.

Alitoa wito kwa maafisa wa serikali za mitaa na wataalamu wa msaada wa kisheria kuendelea kutoa elimu hiyo kwa jamii.




Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe Albert Chalamila amewataka viongozi wa Dini kuendelea kuliombea Taifa amani na kuhubiri masuala ya amani na utulivu wa Nchi ili kuepuka madhara yatokanayo na uvunjifu wa amani hasa katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi mkuu

Akizungumza leo jijini Dar es salaam latika kikao maalum na viongozi wa Dini RC Chalamila amesema viongozi wa dini ni muhimili katika kutunza amani ya nchi huku akisisitiza kuwa serikali kupitia jeshi la polisi itaendelea kuimarisha ulinzi na amewataka watanzania kujifunza madhara ya uvunjifu wa amani kupitia mataifa jirani yenye vurugu

Aidha RC Chalamila ameongeza kuwa hakuna kiongozi anaependa kuona wananchi wake wakikabiliwa na vitendo vya ukatili na uvunjifu wa amani hivyo ni muhimu kwa viongozi wa Dini kusimama imara kupitia madhabahu kwenye nyumba za ibada kuhubiri amani

Kwa upande wa Shekh wa Mkoa wa Dar es Salaam ambae pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya amani ya Mkoa huo Shekh Walid Kawambwa amesema viongozi wa Dini wana nafasi kubwa ya kuimarisha amani na kujenga maadili ndani ya jamii hivyo watumie nafasi zao vizuri huku Mtume Boniface Mwamposa wa makanisa ya Arise and Shine akihimiza viongozi wa Dini kutumia vyema madhabahu kuhubiri amani

Hata hivyo Mkuu wa Wilaya ya Ilala Mhe Edward Mpogolo amesema kuwa viongozi wa dini wamekuwa na mchango mkubwa katika kuombea amani na utulivu wa nchi kwa kushirikiana na makundi mbalimbali ikiwemo wafanyabiashara na bodaboda.









 

Na. Peter Haule,WF, Dar es Salaam
 
Tume ya Mipango itaendelea kushirikiana na Wizara ya Fedha na Taasisi zake katika utekelezaji na ufuatiliaji wa Dira ya Maendeleo 2050 kwa kuwa kazi nyingi za Tume hiyo zinategemea  matokeo ya kazi zinazofanywa na Wizara hususani Ofisi ya Taifa ya Takwimu.

Hayo yamebainishwa na Katibu Mtendaji wa Tume ya Mipango, Dkt. Fred Msemwa, 
alipotembelea Banda la Wizara ya Fedha katika Maonesho ya 49 ya Kimataifa ya Biashara Dar es Salaam (Sabasaba) yanayoendelea katika Viwanja vya Sabasaba, Barabara ya Kilwa, jijini Dar es Salaam.

Alisema kuwa Takwimu mbalimbali za kiuchumi, kijamii na mazingira zitasaidia katika kupanga, kupima, kufuatilia na kufanya tathmini ya  programu za maendeleo wakati wa utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Taifa ya 2050.

Dkt. Msemwa alisema kuwa katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya 2050,Tume itahitaji takwimu na viashiria muhimu  vya mara kwa mara kutoka Ofisi ya Taifa ya Takwimu ikiwa ni pamoja na takwimu rasmi katika maeneo mbalimbali yakiwemo ya  idadi ya watu, pato la taifa na viasihiria vingine vya kiuchumi na kijamii ukiwemo  mfumuko wa bei. 

Aidha, viongozi mbalimbali wa Taasisi na Idara wameendelea kutembelea Banda la Wizara ya Fedha akiwemo Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Chuo cha Mipango ya Maendeleo Vijijini, Prof. Joseph Kuzilwa.

Viongozi wengine ni Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Udhibiti wa Manunuzi ya Umma (PPRA), Bw. Dennis Simba, Mkurugenzi Mtendaji wa Wakala wa Huduma ya Ununuzi Serikalini (GPSA), Prof. Geradine Rasheli, Mkuu wa Chuo cha Mipango ya Maendeleo Vijijini, Prof. Hozen Mayaya, Kamishna Msaidizi wa Idara ya Uendelezaji wa Sekta ya Fedha kutoka Wizara ya Fedha, Bi. Janeth Hiza na Mkurugenzi wa Takwimu za Jamii na Sensa ya Watu Ofisi ya Taifa ya Takwimu, Dkt. Ruth Minja.  

Wengine ni Mkuu wa Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA), Prof. William Pallangyo, Kaimu Mkurugenzi wa TIB Development Bank, Joseph Chilambo, Mkurugenzi wa Hazina Saccos, Dkt. Festo Mwaipaja, Msajili Baraza la Masoko ya Mitaji, Bw. Martin Kolikoli na Katibu Mtendaji wa Baraza la Sanaa Tanzania (BASATA), Dkt. Kedmon Mapama.

Wizara ya Fedha kupitia Idara na Vitengo lakini pia Taasisi zilizo chini ya Wizara, inaendelea kuwakaribisha watanzania kutembelea Banda la Wizara hiyo ili waweze kuhudumiwa. 
Katibu Mtendaji wa Tume ya Mipango, Dkt. Fred Msemwa, akipewa maelezo na Mtakwimu kutoka Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS), Bw. Amri Matole, kuhusu takwimu rasmi na mchango wake katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo, alipotembelea Banda la Wizara ya Fedha katika Maonesho ya 49 ya Kimataifa ya Biashara Dar es Salaam (Sabasaba) yanayoendelea katika Viwanja vya Sabasaba, Barabara ya Kilwa, jijini Dar es Salaam.
Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Chuo cha Mipango ya Maendeleo Vijijini, Prof. Joseph Kuzilwa (kushoto), akipokelewa na  Afisa Habari Mwandamizi kutoka Wizara ya Fedha, Bw. Ramadhan Kissimba,  alipotembelea Banda la Wizara ya Fedha  katika Maonesho ya 49 ya Sabasaba, yanayoendelea katika Viwanja vya Sabasaba, Barabara ya Kilwa, jijini Dar es Salaam, katikati ni Mkuu wa Chuo cha Mipango ya Maendeleo Vijijini, Prof. Hozen Mayaya. 
Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Chuo cha Mipango ya Maendeleo Vijijini, Prof. Joseph Kuzilwa (katikati) na Mkuu wa Chuo cha Mipango ya Maendeleo Vijijini, Prof. Hozen Mayaya, wakisikiliza maelezo kutoka kwa Mkuu wa Idara ya Maendeleo Vijijini na Mipango Miji wa Chuo hicho,Bw. Africanus Sarwatt,  walipotembelea Banda la Wizara ya Fedha  katika Maonesho ya 49 ya Sabasaba, yanayoendelea katika Viwanja vya Sabasaba, Barabara ya Kilwa, jijini Dar es Salaam.
Katibu Mtendaji wa Tume ya Mipango, Dkt. Fred Msemwa (kulia) akisalimiana na Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Udhibiti wa Manunuzi ya Umma (PPRA), walipotembelea Banda la Wizara ya Fedha kwenye Maonesho ya 49 ya Kimataifa ya Biashara Dar es Salaam (Sabasaba) yanayoendelea katika Viwanja vya Sabasaba, Barabara ya Kilwa, jijini Dar es Salaam.Katikati ni Mkuu wa Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA), Prof. William Pallangyo.
Kamishna Msaidizi wa Idara ya Uendelezaji wa Sekta ya Fedha, Wizara ya Fedha, Bi. Janeth Hiza, akiwa katika picha ya pamoja na wataalamu kutoka Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM), alipotembelea Banda la Wizara ya Fedha kwenye Maonesho ya 49 ya Kimataifa ya Biashara Dar es Salaam (Sabasaba) yanayoendelea katika Viwanja vya Sabasaba, Barabara ya Kilwa, jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mtendaji wa Wakala wa Huduma ya Ununuzi Serikalini (GPSA), Prof. Geradine Rasheli, akiwa katika picha ya pamoja na wataalamu Bodi ya Wataalamu wa Ununuzi na Ugavi (PSPTB), alipotembelea Banda la Wizara ya Fedha kwenye Maonesho ya 49 ya Kimataifa ya Biashara Dar es Salaam (Sabasaba) yanayoendelea katika Viwanja vya Sabasaba, Barabara ya Kilwa, jijini Dar es Salaam.
Mtendaji Mkuu wa Hazina Saccos, Dkt. Festo Mwaipaja, akipewa maelezo kuhusu Mifumo ya Fedha kutoka kwa Afisa Mwandamizi wa Idara ya Usimamizi wa Mifumo ya Fedha na Tehama, Bi. Zaina Mwanga, alipotembelea Banda la Wizara ya Fedha kwenye Maonesho ya 49 ya Kimataifa ya Biashara Dar es Salaam (Sabasaba) yanayoendelea katika Viwanja vya Sabasaba, Barabara ya Kilwa, jijini Dar es Salaam.
Katibu Mtendaji wa Tume ya Mipango, Dkt. Fred Msemwa akiteta jambo na Kaimu Kamishna wa Kitengo cha Ubia kati ya Sekta ya Umma na Binafsi kutoka Wizara ya Fedha, Bw. Bashiru Taratibu, alipotembelea Banda la Wizara ya Fedha kwenye Maonesho ya 49 ya Kimataifa ya Biashara Dar es Salaam (Sabasaba) yanayoendelea katika Viwanja vya Sabasaba, Barabara ya Kilwa, jijini Dar es Salaam.
Katibu Mtendaji wa Tume ya Mipango, Dkt. Fred Msemwa (wa kwanza kushoto) na Kaimu Mkurugenzi wa TIB Development Bank, Joseph Chilambo (wa pili kushoto), wakisikiliza maelezo kuhusu Benki hiyo katika kuchochea maendeleo ya uchumi, walipotembelea Banda la Wizara ya Fedha kwenye Maonesho ya 49 ya Kimataifa ya Biashara Dar es Salaam (Sabasaba) yanayoendelea katika Viwanja vya Sabasaba, Barabara ya Kilwa, jijini Dar es Salaam.

(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Fedha)


 

Mwanafunzi wa mwaka wa tatu wa Shahada ya Awali ya  Sayansi  katika Mifumo ya Habari za Afya ( HIS) kutoka  Shule Kuu ya Uuguzi na Afya ya Jamii (SoNPH) Bw. Lucas Allen Haule ameibuka Mshindi  wa Kwanza wa bunifu ya Utengenezaji wa Nembo ya Made in Tanzania ambapo lilihusisha zaidi ya washiriki 80 nchini Tanzania.


Shindano hilo lililaratibiwa na Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania ( TANTRADE) na leo tarehe 8 Julai  katika Ukumbi wa Karume "Sabasaba" amekabidhiwa zawadi ya Ushindi na Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Exaud Kigahe ( Mb). 
Aidha; Nembo hiyo ilizunduliwa Rasmi tarehe 7 Julai, 2025 na  Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dkt.Hussein Mwinyi wakati wa Ufunguzi wa Maonesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba).



Pamela Mollel,Arusha.

Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2025, Ndugu Ismail Ally Ussi, amezitaka sekta binafsi nchini kutumia vema fursa ya uboreshaji wa sera na mazingira ya uwekezaji nchini .

Amesema kuwa serikali ya awamu hii imefanya kazi kubwa ya kuondoa vikwazo vingi vya uwekezaji ili kuvutia wadau wengi kufanya kazi na biashara nchini.

Ussi ameyasema hayo baada ya kuzindua kituo cha kisasa cha mafuta cha Petro Africa (T) Ltd kilichojengwa kwa gharama ya zaidi ya Shilingi 800 milioni wilayani Longido, mkoani Arusha walipotembelea na msafara wa mwenge wa Uhuru.

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi rasmi wa kituo hicho kilichojengwa katika Kata ya Kimokouwa, Ussi amesema kuwa kuwa mradi huo ni ushahidi wa namna sekta binafsi inavyoweza kushiriki kikamilifu katika jitihada za kitaifa za maendeleo.

“Nawapongeza kwa uwekezaji huu wa mfano kwani mmeonesha uzalendo wa hali ya juu na mmejitokeza kuwa sehemu ya historia ya Mwenge wa Uhuru kwa vitendo”amesema na kuongeza;

“Hii ni njia mojawapo ya kumuunga mkono Rais wetu Dk Samia Suluhu Hassan katika juhudi zake za kuboresha mazingira ya uwekezaji nchini, hivyo niwaombe na wengine wahakikishe wanatumia fursa hii vuzuri” amesema Ussi.

Mbali na hilo, Ussi amewataka wananchi wa wilaya ya Longido kuwaunga mkono wawekezaji wanaojitokeza kutatua kero mbalimbali katika jamii zao ikiwemo kununua bidhaa wanazoleta.

“Hapa amejitokeza muwekezaji huyu kajenga kituo hiki ambacho kitaondoa kero ya upatikanaji wa mafuta, niwaombe mje kununua mafuta hapa, maana hadi kuita mwenge wa uhuru kuzindua maana yake mafuta yake yako safi na yana viwango vya hali ya juu” amesema.

Akisoma taaarifa ya mradi huo mbele ya wakimbiza mwenge kitaifa na viongozi wa serikali, Meneja wa Kanda ya Kaskazini wa PetroAfrica (T) Ltd, Abdi Hassan Ibrahim, amesema mradi huo ulianza kutekelezwa Machi 2024 na kukamilika mwezi Juni 2025, kwa gharama ya shilingi milioni 800.

Amesema ujenzi huo umehusisha visima vya kuhifadhia mafuta, pampu za kisasa, maeneo ya maegesho, ofisi za kisasa, pamoja na miundombinu ya usalama.

“Lengo ni kuongeza wigo wa upatikanaji wa huduma za nishati ya mafuta kwa wananchi na sekta ya usafirishaji, sambamba na kuchochea maendeleo ya kiuchumi katika eneo la mpakani mwa Tanzania na Kenya”.

“Tunashukuru Serikali ya awamu ya sita kwa mazingira bora ya uwekezaji yaliyopelekea kufanikisha mradi huu. Mbali na kuongeza huduma ya nishati, tumetoa ajira kwa wananchi wa Longido na kusaidia taasisi za umma na sekta binafsi kupunguza changamoto za upatikanaji wa mafuta,” amesema Ibrahim.

Mkurugenzi wa Vodacom Tanzania , Philip Besiimire ( Mwenye tisheti nyeupe), pamoja na Mkurugenzi wa Udhibiti wa Hatari na Utii wa Sheria Agapinus Tax,( wa kwanza kushoto) wakipewa maelekezo kuhusu televisheni janja (smart screen) inayotoa maelekezo kuhusu bidhaa mbalimbali zinazopatikana katika banda la kampuni hiyo lililoko katika viwanja vya sabasaba ambako maonesho ya 49 ya kimataifa ya Dar es Salaam yanaendelea.

shughuli za kuhamasisha wateja kwenye maonesho ya Sabasaba. Tukio Hilo limetokea leo , katika maadhimisho ya siku ya sabasaba jijini Dare es salaam.




Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Mahmoud Thabit Kombo (Mb.) ameshiriki Kongamano kuhusu Kukuza Huduma za Afya Ulimwenguni kupitia Diplomasia lililoandaliwa na Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi, Muhimbili (MUHAS) jijini Dar es Salaaam Julai 8, 2025.

Waziri Kombo ameeleza kuwa Sera ya Mambo ya Nje ya Mwaka 2001 toleo la mwaka 2024 iliyozinduliwa tarehe 19 Mei, 2025 na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ilienda sambamba na uzinduzi wa Kitabu cha Mwongozo wa Diplomasia ya Uchumi kinachoeleza utekelezaji wa Diplomasia katika sekta mbalimbali ikiwemo ya afya.

Ameeleza kufurahishwa na wanafunzi wa MUHAS kwa kujipambanua mapema katika diplomasia ya afya kwani Tanzania sasa imekuwa kivutio kwa wengine kuja nchini kupata huduma mbalimbali za afya.

Hatua hii imesaidia kupunguza gharama ya kupeleka wagonjwa kutibiwa nje ya nchi. Hivyo, Kongamano hilo limelenga kuieleza Afrika na Dunia kuwa Muhimbili ipo tayari kuwahudumia kwa huduma bora na utaalamu wa hali ya juu.

Aidha, katika muendelezo wa kutekeleza Sera ya Mambo ya Nje kwa vitendo, Wizara pia ilishiriki mwaliko wa Mkuu wa Mkoa wa Dodoma kwenye kongamano lililofanyika mwezi Juni 2025, Dodoma kwa lengo la kutangaza fursa mbalimbali zilizopo mkoani humo ikiwemo huduma ya afya, elimu, biashara, uwekezaji na utalii kwa Mabalozi wote wanaowakilisha nchini.















Top News