Na Munir Shemweta, CHALINZE

Katibu Mkuu wa Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhandisi Anthony Sanga amesema Hati miliki za Ardhi zinazotolewa kwa wamiliki wa ardhi nchini haziruhusiwi kuwekewa ‘’Lamination’’.

Mhandisi Sanga ametoa kauli hiyo tarehe 18 Machi 2024 wilayani Chalinze mkoa wa Pwani wakati wa ziara ya Kamati ya Kudumu ya Ardhi Maliasili na Utalii kukagua utekelezaji Mradi wa Kupanga, Kupima na Kumilikisha Ardhi (KKK) katika eneo la Msolwa .

‘’Hati unayopewa mwananchi hautakiwi kuifanyia lamination, kwanza ijulikane zipo hati za zamani zilizowekewa kitabu kama majalada na zile mpya’’ alisema Mhandisi Sanga.

Kwa mujibu wa Katibu Mkuu wa wizara ya ardhi, mmiliki wa ardhi anaweza kutaka kuuza ardhi ama nyumba yake kwa mtu mwingine ama kutaka kuchukulia mkopo hivyo hati yake inabidi igongwe muhuri na kama ikifanyiwa ‘’lamination’’ itakuwa ngumu kugongwa muhuri.

Kwa mantiki hiyo, Mhandisi Sanga ameweka wazi kuwa, ndiyo maana wizara yake ya ardhi inashauri hati miliki za ardhi zisifanyiwe ‘’lamination’’ ili mmiliki anapotaka kufanya muamala wowote basi hati yake iweze kufanyiwa.

‘’Lakini hata zile hati milki mpya za kieletroniki hali kadhalika, maana hata hizo zina ‘electronic feature’ .mle ndani yaani kuna vitu vinavyofanya iwe hati ya  kipekee lakini pia ina bacon, mambo ya kisasa kidogo hiyyo ukifanya ‘’lamination’’ mambo yote hayo huwezi kuyafanya’’ alisema Mhandisi Sanga.

Amebainisha kuwa, wizara yake ya ardhi itaendelea kutoa elimu juu ya suala hilo sambamba na kutoa maagizo kwa watendaji wote wa sekta ya ardhi kuweka matangazo kwenye ofisi zao kuhakikisha wananchi wanapata elimu kwamba hati milki ya ardhi haitakiwi kufanyiwa ‘’lamination’’ iwe mpya au ya zamani ili kumsaidia mwananchi mwenye hati kufanya muamala anaotaka kufanya.

Kamati ya Kudumu ya Ardhi Maliasili na Utalii imehitimisha kutembelea na kukagua miradi ya Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi tarehe 18 Machi 2024 ambapo katika ziara zake imeweza kukagua mradi wa Uboreshaji Usalama wa Milki za Ardhi (LTIP) katika Halmashauri ya wilaya ya Ruangwa mkoa wa Lindi, Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni Dar es Salaam pamoja na mradi wa Kupanga, Kupima na Kumilikisha ardhi katika eneo la Msolwa lililopo Halmashauri ya Chalinze mkoa wa Pwani.Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhandisi Anthony Sanga (Kulia) akisalimiana na Mjumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi Maliasili na Utalii wakati wa ziara ya Kamati hiyo mkoani Pwani.Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhandisi Anthony Sanga (Kulia) mara baada ya kuwasili Ofisi ya Mkuu wa mkoa wa Pwani wakati wa ziara ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi Maliasili na Utalii mkoani humo. 

Na Mwandishi Wetu


KAMPUNI ya Geita Gold Mining Limited (GGML) imetoa mafunzo maalumu kwa wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Wavulana Geita (Geita Boys) kwa lengo la kuwawezesha wanafunzi hao kutambua masomo sahihi wanayoyamudu na fani zinazoendana na masomo hayo katika soko la ajira.

Mafunzo hayo yametolewa wiki iliyopita mkoani Geita na baadhi ya wafanyakazi wa GGML wakiwamo wanawake wanaounda kundi la GGM Ladies ikiwa ni mwendelezo wa maadhimisho ya sherehe za siku ya wanawake duniani.

GGML ladies imetoa mafunzo hayo ya siku moja kupitia program maalumu ya ushauri na usimamizi iliyopewa jina la (GGM Mentorship Program) kwa lengo la kuwawezesha wanafunzi hao wa kidato cha kwanza hadi cha tano, kutambua uwezo wao kielimu na malengo waliyojiwekea katika kutimiza ndoto zao.

Akizungumza na wanafunzi hao, Ofisa wa masuala ya usafirishaji kutoka idara ya Rasilimali watu, Laila Mohamed alisema huu sio muda wa wanafunzi kufuata mkumbo katika kuchagua masomo ya kusoma na kufikia malengo yao kimaisha.

“Ili kufikia malengo ya kitaaluma, hiki sio kipindi cha kufuata mkumbo... kwamba ukisikia Juma amechukua biology na wewe unachukua mchepuo wa sayansi. Hiki ni kipindi cha kujitathmini na kujitafakari kwamba ni kitu gani unakimudu ili uchukue masomo sahihi kufikia lengo lako,” alisema.

Alisema wanafunzi wengi wamekuwa na changamoto ya kutokuwa na msimamizi au mshauri anayeweza kuwashauri namna ya kujinasua katika changamoto mbalimbali kitaaluma jambo ambalo GGML imeona ni vema kujaza nafasi hiyo.

Kwa upande wake Joscar Rumanyika ambaye ni Mhasibu kutoka GGML, aliwaonya wanafunzi hao kujiepusha na vitendo viovu vya uvunjifu wa maadili ili kutimiza malengo yao kitaalumu.

Amewataka wataka wanafunzi hao kuwa na uthubutu na kujiamini kwamba hakuna kinachoshindikana ili kufaulu vema katika masomo yao.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti baadhi ya wanafunzi hao kutoka Geita Boys, Leonard Martin na Daniel Stanslaus walisema mafunzo waliyopatiwa na GGML yamewasaidia kutambua namna ya kufikia malengo yao.

Martin (14) ambaye ni mwanafunzi wa kidato cha pili na mkazi wa Bwanga mkoani Geita, alisema alisema elimu hiyo inawawezesha kujiandalia maisha mazuri ya baadae.

Makamu Rais Mwandamizi wa AngloGold Ashanti-GGML - Kitengo cha Ubisa/ Ushirika Afrika, Terry Stron alisema program hiyo ya mentorship inalandana na malengo ya kampuni hiyo ya kuwekeza kwa vizazi vijavyo kwani kuwekeza kwa wanafunzi hao ni sawa na kuwekeza kwa jamii ya Geita ijayo.

 

 Na Mwamvua Mwinyi,Pwani

Mbunge wa jimbo la Chalinze, Ridhiwani Kikwete amekabidhi pikipiki 6 kwa Maafisa Ugani wa Halmashauri wa Halmashauri ya Chalinze ikiwa ni sehemu ya kuendelea kuwapatia Vitendea kazi Watumishi kwenye sekta ya Kilimo na Mifugo .

Akikabidhi Pikipiki hizo , Ridhiwani ameeleza, zimetolewa na Serikali Kuu kupitia Wizara ya Kilimo na zinalenga kuwawezesha  maafisa Ugani kuweza kufika katika maeneo na kwa wenye uhitaji ili kuboresha sekta ya kilimo ."Kugawiwa kwa pikipiki hizi kunafanya maafisa ugani waliopewa vifaa hivi kufika 14 kati ya kata 16 za Halmashauri hii".

Halmashauri ya Chalinze ni moja kati ya Halmashauri zinazoongoza kwa kilimo katika eneo la Mashariki ya Tanzania.





 

 


Na Munir Shemweta, CHALINZE

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi Maliasili na Utalii imesema kuwa, haijaridhishwa na urejeshaji mikopo ya fedha za mradi wa kupanga, kupima na kumilikisha ardhi (KKK) unaofanyika kwenye halmashauri mbalimbali nchini.

Hayo yamebainishwa leo tarehe 18 Machi 2024 na Kamati hiyo wakati ilipotembelea na kukagua utekelezaji mradi wa Kupanga, Kupima na Kumilikisha Ardhi (KKK) katika eneo la Msolwa katika halmashauri ya wilaya ya Chalinze mkoa wa Pwani.

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi Maliasili na Utalii Mhe, Timotheo Mzava ameeleza kuwa, mbali na Kamati yake kuridhishwa na mradi wa KKK kwa ujumla lakini hawajaridhishwa na namna mikopo hiyo inavyorejeshwa na halmashauri.

Akitolea mfano wa Halmashauri ya Chalinze katika mkoa wa Pwani, Mhe, Mzava amesema pamoja na halmashauri hiyo kukopeshwa kiasi cha shilingi Bilioni 2.5 kwa ajili ya mradi wa KKK lakini imeshindwa kurejesha fedha kwa wakati.

 ‘’Kama Kamati bado hatujaridhishwa kabisa namna ya kasi ya urejeshaji fedha hizi na wito na msisitizo wetu zifanyike kila aina ya jitihada kuhakikisha fedha zinarudi ili zikasaidie maeneo mengine yenye uhitaji ili dhamira ya Rais ya kutoa fedha hizo iweze kufikiwa’’ alisema Mzava

Kwa mujibu wa Mhe, Mzava, hadi Machi 2024 kwa ujumla wizara imepokea marejesho ya shilingi bilioni 22.7 kati ya shilingi bilioni 50 sawa na asilimia 45 kutoka kwenye halmashauri na taasisi mbalimbali zilizonufaika na mkopo huo.

Amesema, fedha zinazotolewea kama mkopo usio na riba kwa halmashauri zikirejeshwa zitasaidia kukopesha halmashauri nyingine na hivyo kuisaidia kutatua changamoto za sekta ya ardhi nchini na kuboresha katika maeneo mengine.

Hata hivyo, ametaka kufanyika jitihada mbalimbali ili kusaidia katika urejeshaji mikopo hiyo na kuweza kuzisaidia halmashauri nyingine ili ziweze kuondoa changamoto za sekta ya ardhi nchini.

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe, Geophrey Pinda amebainisha kuwa, mpaka sasa halmashaurii zilizorejesha kiasi chote cha fedha ya mkopo ni 12 huku zile zilizorejesha sehemu ya fedha zikiwa ni 43.

Mhe, Pinda amesema, Programu ya Kupanga, Kupima na Kumilikisha Ardhi (KKK) ni program ya miaka kumi inayotekelezwa na wizara yake kwa kushirikiana na halmashauri mbalimbali nchini.

Ameongeza kuwa, utekelezaji wa Programu hiyo ulianza mwaka 2018/2019 na unatarajiwa kukamilika 2028/2029. Lengo la Programu ya KKK ni Kupanga miji na kuhakikisha makazi holela yanaondolewa kwenye maeneo mbalimbali nchini.

Programu hiyo inatekelezwa na Serikali kwa kushirikiana na Halmashauri ambazo ni mamlaka za upangaji na sekta binafsi ambapo program hiyo inagharimiewa na serikali kupitia fedha za ndani za bajeti ya maendeleo.

Serikali ilitoa mtaji wa shilingi Bilioni 50 kwa ajili ya utekelezaji wa program ya KKK kwa utaratibu wa kuzikopesha halmashauri na taasisi ambapo wizara kwa kushirikiana na wizara ya fedha na Ofisi ya Rais TAMISEMI ziliweka utaratibu kwa kuweka vigezo vya kutoa mkopo huo bila riba kwa ajili ya utekelezaji wa program.

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi Maliasili na Utalii Mhe, Timotheo Mzava akisalimiana na Mkuu wa Wilaya ya Kibaha Nickson Simon mara baada ya Kamati yake kuwasili mkoa wa Pwani kukagua utekelezaji Mradi wa Kupanga, Kupima na Kumilikisha Ardhi katika halmashauri ya Chalinze mkoa wa Pwani tarehe 18 Machi 2024. Katikati ni Naibu Waziri wa Ardhi Mhe, Geophrey Pinda.
Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe, Geophrey Pinda akisalimiana na Mbunge wa Jimbo la Chalinze na Naibu Waziri Ofisi ya Rais Menejiment ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe, Ridhiwani Kikwete wakati wa ziara ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi Maliasili na Utalii katika halmashauri ya wilaya ya Chalinze Machi 18, 2024.
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Ardhi Maliasili na Utalii Mhe, Timotheo Mzava na Naibu Waziri wa Ardhi Mhe, Geophrey Pinda wakimsikiliza Afisa Ardhi wa Halmashauri ya wilaya ya Chalinze Deo Msilu (wa pili kulia) kuhusu mradi wa Kupanga, Kupima na Kumilikisha Ardhi unaotekelezwa katika eneo la Msolwa Halmashauri ya Chalinze Machi 18, 2024.
Afisa Ardhi wa Halmashauri ya wilaya ya Chalinze Deo Msilu akisisitiza jambo mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi Maliasili na Utalii ilipokwenda kukagua mradi wa Kupanga, Kupima na Kumilikisha Ardhi katika eneo la Msolwa Chalinze Machi 18, 2024.
Afisa Ardhi wa Halmashauri ya wilaya ya Chalinze Deo Msilu (Kulia) akielezea matumizi ya kifaa cha upimaji mbele ya wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi Maliasili na Utalii ilipokwenda kukagua mradi wa Kupanga, Kupima na Kumilikisha Ardhi katika eneo la Msolwa Chalinze Machi 18, 2024.
Mbunge wa jimbo la Chalinze na Naibu Waziri Ofisi ya Rais Menejiment ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe, Ridhiwani Kikwete akimkabidhi Hati Milki ya Ardhi mmoja wa wananchi wa Chalinze wakati wa ziara ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi Maliasili na Utalii ilipokwenda kukagua mradi wa Kupanga, Kupima na Kumilikisha Ardhi eneo la Chalinze machi 18, 2024. (PICHA ZOTE NA WIZARA YA ARDHI)

 



Na Said Mwishehe, Michuzi TV


WAKALA wa Huduma za Misitu Tanzania(TFS)umesema katika kipindi cha miaka mitatu ya uongozi wa Rais Dk.Samia Suluhu Hassan umefanikiwa katika mambo mengi yakiwemo ya kuimarisha sekta ya uhifadhi ,ujenzi wa miundombinu na kutoa ajira kwa askari na maofisa zaidi ya 500.

Akizungumza na waandishi wa habari kuhusu miaka mitatu ya Rais Dk.Samia Suluhu Hassan, Kamishina wa Uhifadhi wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania(TFS)Profesa Dos Santos Silayo amesema  katika kipindi cha miaka mitatu ya Rais Dk.Samia Suluhu Hassan wanajivunia uongozi wake ambao unajali na kuthamini uhifadhi.

“Tunatoa shukrani na kumpongeza Rais Dk.Samia Suluhu Hassan kwa kutimiza miaka mitatu na katika jambo ambalo sekta ya misitu tunajivunia katika uongozi wake ni kuwa na kiongozi wa juu anayejali na kuthamini uhifadhi.

“Anatoa msukumo wa moja kwa moja yeye binafsi kwenye hilo tunamshukuru sana Rais Dk.Samia kwani katika kipindi cha miaka mitatu ya uongozi wake tumefanikiwa kuimarisha uhifadhi wa misitu na misitu yetu imeendelea kushamiri,”amesema.

Ameongeza kuwa TFS wameongeza wigo  wa upandaji miti ya aina mbalimbali lakini katika kipindi hicho cha miaka mitatu yeye mwenyewe Rais Samia anavyozungumzia suala la uhifadhi na utalii amekuwa akitoa mchango wa moja kwa moja kuhamasisha jamii ile dhana na nia ya uhifadhi wa mazingira.

Amesema Rais Samia amekuwa akijali  viumbe hai kwa kuwa yeye mwenyewe anajali na anatekeleza kwa vitendo jambo hilo, kwa hiyo wanamshukuru Rais.“Ametusidia sana maeneo ya utalii tumefanya vizuri.

“Ametuongezea nguvu katika kupata maofisa na askari wa kulinda misitu yetu tumeajiri takriban askari 500 katika kipindi cha miaka mitatu ya uongozi wa Rais Samia.Tumeboresha miundombinu yetu kwa ajili ya kupata ofisi na makazi ya maofisa na askari wetu,”amesema Prof.Silayo.

Aidha amesema  kwa kipindi cha miaka mitatu peke yake wamewekeza Sh.bilioni 31 ambazo zimesaidia kujenga ya ofisi 88 kote nchini ya ofisi lakini wamenunua magari na mitambo ya kutosha.

“Takriban Sh.bilioni 18 zimetumika katika kipindi cha miaka mitatu na tumepata magari kwani tunayo magari  madogo 113, mitambo 17, boti 10 na pikikipiki 164 katika kipindi cha miaka mitatu.

“Kwa kweli ni uwekezaji mkubwa umefanyika ambao katika hali ya kawaida usingeweza kuwepo lakini Rais kwa maelekezo yake ya moja kwa moja au kwa marekebisho ya mifumo mbalimbali imetuwezesha kufikia mafanikio haya kama taasisi, hivyo tunamshukuru Rais Dk.Samia,”amesisitiza

Pia ameongeza katika kipindi cha miaka mitatu ya uongozi wa Rais Samia, TFS imeongeza ushirikishaji wa wananchi katika uhifadhi na utunzaji wa misitu kwani wao ndio wanaona faida ya moja kwa moja ya uwepo wa misitu hiyo.

Amesisitiza katika kusimamia rasilimali za misitu changamoto kubwa inakuja pale ambapo kunakuwa hakuna ushirikishwaji wa wananchi ambao ndio wasimamizi wa awali , hivyo TFS wameongeza nguvu katika kushirikisha wananchi

“Tunawashirikisha kwa kuwapa elimu kupitia vipindi vya kutoa elimu kwa umma katika televisheni , pia tunawapa elimu kuhusu umuhimu wa uhifadhi wa misitu na katika kuwavutia tumekuwa na miradi mbalimbali kwa wananchi kwa lengo la kutia hamasa.

“Kumekuwa na  miradi kama ufugaji nyuki, lakini wengine ukuzaji wa miche ambapo tunawasaidia miche, hivyo wanakuza miche na kuuza katika maeneo yao.Pia tunawasaidia katika ujenzi wa madarasa , ofisi za walimu maabara na mabweni.

“Tumekuwa tukisaidia sekta ya afya kwa kuboresha miundombinu ukiwemo wa ujenzi wa zahanati kwa mfano kule kijiji cha Wachawaseme tumejenga hospitali yenye thamani ya Sh.milioni 274.Tunagawa miti kwa wananchi ambayo thamani yake ni takriban Sh.bilioni sita kwa mwaka ambayo tunawapa bure wananchi,”amesema.

Ameongeza wamekuwa wakiwashirikisha  wananchi kwa kuwapa mbinu za kupambana na majanga katika maeneo ya misitu kwani kuna misitu yao ambayo inapata majanga ya moto, hivyo tunawashirikisha wananchi namna ya kupambana na majanga hayo.

Na Mwandishi wetu, NCAA.

Makamu mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Ngorongoro ambaye pia ni Diwani wa kata ya Olbalbal iliyopo ndani ya hifadhi ya Ngorongoro Mhe. Emmanuel Tonge ni miongoni mwa wananchi 463 waliohama kutoka ndani ya hifadhi ya Ngorongoro kwenda Kijiji cha Msomera na maeneo mengine.

Hafla ya kuwaaga wananchi wanaohama kwa hiari imefanyika leo tarehe 19 machi, 2024 na kuongozwa na mkuu wa Wilaya ya Ngorongoro Kanali Wilson Sakulo ambapo jumla ya kaya 77 zenye watu 463 na mifugo 1,408 wamehama ndani ya hifadhi hiyo baada ya kujiandikisha kuhama kwa hiari.

Diwani wa kata ya Olbalbal ambaye pia ni Makamu mwenyekiti wa Halmashauri ya Ngorongoro na katibu wa baraza la wafugaji Ngorongoro amesema ameamua kuhama baada ya kuona dhamira ya Serikali ya awamu ya 6 kuboresha huduma bora za kijamii nje ya hifadhi na kurahisisha mazingira ya uandikishaji kwa kuwafuata wananchi kwenye ofisi za vitongoji, vijiji na kata kuwapatia elimu ya kutosha kuhusu uwepo wa maisha bora ndani ya hifadhi.

“Ndani ya hifadhi hakuna kesho iliyobora kwa watoto wangu, Serikali ikaona itenge maeneo rasmi na kujenga huduma za kijamii kama shule, vituo vya afya, zahanati, maji safi, barabara, mawasiliano ya simu, posta, majosho, eneo la malisho na mashamba ya kutosha kwa kilimo, kwa fursa hii sina haja ya kuendelea kushi na Wanyama ndani ya hifadhi” ameongeza Mhe. Tonge.

Meneja mradi wa kuhamisha wananchi wanaohama kwa hiari Ngorongoro Afisa Uhifadhi Mkuu Flora Assey ameeleza kuwa hadi kufikia wiki hii jumla ya kaya 1,195 zenye watu 7,195 na mifugo 33,064 zimeshahama ndani ya Hifadhi.

Ameongeza kuwa kati ya kaya 77 zilizohama ndani ya hifadhi wiki hii, kaya 75 zimeenda Kijiji cha Msomera Wilaya ya Handeni na kaya mbili (02) zimehamia kijiji cha Makao Meatu Mkoani Simiyu.

Naibu Kamishna wa Hifadhi huduma za Shirika NCAA Salum Mjema amebainisha kuwa Serikali imeendelea kuboresha zoezi la utoaji elimu, uandikishaji na uthaminishaji kwa kuongeza timu ya uandikishaji ambapo ndani ya mwezi mmoja taratibu zote ikiwepo malipo zinakuwa zimekamilika na wananchi kuhamishwa bila kusiburi mda mrefu.

Mjema ameongeza kuwa ujenzi wa nyumba za makazi 2,500 katika Kijiji cha Msomera unaendelea kwa kasi ambapo nyumba 903 zimeshakamilika, nyumba 97 zipo katika hatua za umaliziaji, nyumba 1500 zipo kwenye hatua mbalimbali za ujenzi huku maandalizi ya ujenzi wa nyumba zingine 2500 yakiendelea katika vijiji vya Kitwai Wilani Simanjiro na Saunyi wilaya ya Kilindi.

Katika hatua nyingine mkuu wa Wilaya ya Ngorongoro Kanali Wilson Sakulo ametoa wito kwa jamii kupuuza baadhi ya watu wanaopotosha kuwa baadhi ya wananchi wanaohamishwa ndani ya hifadhi sio wakazi wa Ngorongoro na kusisitiza kuwa serikali iko macho na makini katika utekelezaji wa zoezi kwa kuhakikisha wananchi wote wanaojiandikisha kuhama kwa hiari ni wakaazi wenyeji wanaoishi ndani ya eneo la hifadhi ya Ngorongoro lenye vijiji 25 na kata 11 na si vinginevyo.







Na Said Mwishehe,Michuzi TV

NCHI zaidi ya 50 zinatarajia kushiriki katika Kongamano la 10 la Jotoaridhi Afrika(ARGeo-C10) linalotarajia kufanyika Novema mwaka huu ambapo Tanzania tayari imezindua maandalizi ya kuandaa Kongamano hilo linalotarajia pia kushirikisha wadau mbalimbali.

Akizungumza leo Machi 18,2024 Jijini Dar es Salaam wakati wa Tanzania ikizindua maandalizi ya Kongamano hilo, Kamshina wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Innocent Luoga amesema Kongamano hilo litafanyika kuanzia Novemba 11 hadi Novemba 17 mwaka huu 

Akifafanua zaidi ameeleza kwamba nchi 50 zikiwemo wanachama wa ARGeo ambazo ni Tanzania, Kenya, Uganda, Rwanda, Ethiopia na Djibout zitashiriki na washiriki watakaohudhuria ni zaidi ya watu 1000.

"Katika kongamano hilo zaidi ya watu 1,000 wa kada mbalimbali zinazohusiana na sekta hiyo muhimu katika kuzalisha nishati safi na salama wanatarajiwa kushiriki."

Akieleza zaidi Mhandisi Luoga amesema mwaka 2022 Rais Dk.Samia Suluhu Hassan alikubali ombi la Shirika la Mazingira la Umoja wa Mataifa (UNEP) kufanyika kwa kongamano hilo, hivyo kwa sasa Tanzania inaendelea na maandalizi ili liweze lifanye na leo ndio umefanyika uzinduzi rasmi wa maandalizi ya Kongamano hilo.

Ameongeza Serikali kupitia Kampuni ya Uendelezaji Jotoardhi Tanzania (TGDC) itashirikiana na UNEP kuhakikisha kongamano hilo muhimu linafanikiwa kwa kiwango kikubwa, ili dhamira ya serikali kuongeza nishati jadidifu inafikiwa.

Pia amesema kongamano hilo ni muhimu kwa Tanzania kutokana na kuwa na rasilimali nyingi za jotoardhi, hivyo matumaini yao ni kuwa washiriki wataweza kujifunza na kubadilishana taaluma.

"Tunatarajia wataalam, wawekezaji, wafanyabiashara na viongozi mbalimbali ambao watashiriki Kongamano hilo la Jotoaridhi watapata nafasi ya kuchochea kasi ya uzalishaji nishati hii kupitia majadiliano na maazimio yatakayotolewa wakati wa Kongamano."

Kuhusu rasilimali ya jotoaridhi, Mhandisi Luoga amesema ulianza kufanyiwa utafiti tangu mwaka 1970 hivyo kwa sasa wanaendelea na utekelezaji wa kuzalisha kupitia TGDC ambapo wameanza kwenye baadhi ya maeneo kati ya 51 yanayoweza kuzalisha nishati hiyo.

"Kwa mujibu wa tafiti zilizopo zinaonesha Tanzania inaweza kuzalishaji megawati 5,000 za umeme wa jotoardhi na tunaendelea kutekeleza miradi ambayo inatarajiwa kuzalisha megawati 200 ifikapo mwaka 2027."

Aidha amesema kuna maeneo matano ambayo tumeyaainisha kwa ajili ya uzalishaji wa nishati ya jotoardhi ambayo ni Ngozi(megawani 70), Kiejo Mbaka(megawati 60) , Natron (megawati 60), Songwe (megawati tano)na Ruoyi Kisaki (megawati tano) hadi kufikia megawati 200.

Kwa pande wake Meneja wa TGDC, Mhandisi Mathew Mwangomba amefafanua kongamano hilo la 10 ambalo litafanyika nchini Tanzania limekuja wakati muafaka kwania dunia ipo katika mapambano ya kupunguza hewa ukaa ambayo imekuwa na madhara makubwa kwenye mazingira na kuongeza Nishati itokanayo na Jotoaridhi ni rafiki wa mazingira.

Pia amesema upatikanaji wa jotoardhi nchini unaendana na hatua tatu muhimu ambazo ni sayansi jiolojia, jiofizikia na jiokemia ambayo ipo nchini kupitia Bonde la Ufa la Magharibi, Mashariki na Kusini ambayo kitalaam wanaiita Tripple Juction.

Ameeleza pia  TGDC wanatekeleza Ngozi kuchimba nishati ya jotoardhi ambayo inapatikana kwa nyuzi joto 250, hivyo basi kukutana kwa wadau 1,000 kujadili jotoardhi tunaenda kupiga hatua zaidi,” alisema.

Awali Mwakilishi Mkazi wa UNEP Tanzania, Clara Makenya  amesema kwamba wanatarajia kongamano hilo litatoa mwanga kwa duania kuwekeza katika nishati safi na salama kama jotoardhi na kuachana na nishati ambazo zina madhara kwa jamii na mazingira.





Uzinduzi wa kongamano la jotoardhi la kikanda Afrika ambalo linatarajiwa kufanyika Novemba 11 hadi 17, 2024  katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa Julius Nyerere (JNICC), jijini Dar es Salaam, ambapo washiriki zaidi ya 600 wanatarajiwa kuhudhuria mkutano huo, ni mara ya pili Tanzania kuwa mwenyeji wa mkutano huo uliofanyika 2014 jijini Arusha kwa mara ya kwanza.

Na Mwandishi Wetu, Barcelona 


UBALOZI  wa Tanzania nchini Ufaransa ambao unawakilisha pia nchini Uhispania, kwa kushirikiana na Bodi ya Utalii Tanzania (TTB), umeratibu na kuongoza ushiriki wa makampuni kadhaa ya utalii kutoka Tanzania katika Maonesho ya Utalii ya B-Travel yaliyoanza Machi 15 Machi, 2024, mjini Barcelona, Falme ya Uhispania.

Taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari na Ubalozi huo imesema kwamba maonesho hayo ya siku tatu yana lengo la kuwawezesha wenyeji wa Barcelona wenye wa asili ya Catalunya (Catalans) ambao wana desturi ya kutembelea kwa wingi maonesho hayo kutafuta maeneo ya kutembelea wakati wa majira ya kiangazi yanayokaribia kuanza. 

Wakati wa ufunguzi, Waziri wa Biasahara na Kazi Roger Torrent i Ramio alitembelea banda la Tanzania na kushukuru kwa ushiriki wa Tanzania kwa kueleza  Tanzania na Zanzibar ni maeneo yanayovutia watu wengi kuyatembelea kwa sasa na kwamba anategemea mafanikio makubwa ya Tanzania katika sekta ya utalii.

Na Mwandishi wetu, Babati


MKUU wa mkoa wa Manyara, Queen Cuthbert Sendiga amesema huduma za afya zimeboreshwa hivi sasa eneo hilo ndiyo sababu wagonjwa na majeruhi wa maafa yaliyotokea Hanang' walitibiwa Manyara.

Maporomoko ya tope kutoka mlima Hanang' yalitokea Desemba 3 mwaka 2023 na kusababisha vifo vya watu 89, wengine kujeruhiwa na wengine kukosa makazi.

Maafa hayo yalitokea jumapili alfajiri na kuathiri miundombinu ya mji mdogo wa Katesh na maeneo ya karibu ya Gendabi, Jorodom, Ganana, Sarijandu na Dumbeta.

Sendiga akizungumza mjini Babati kwenye kikao cha ushauri cha mkoa huo (RCC) amesema wagonjwa na majeruhi, walitibiwa Manyara kwani hawakusafirishwa ila madaktari bingwa ndiyo walikuja Manyara.

Amesema wagonjwa na majeruhi wa maafa ya Hanang' walitibiwa Manyara, kutokana na huduma bora za afya kuboreshwa ikiwemo kuwepo kwa vifaa tiba na dawa.

"Tukiwa tunaadhimisha miaka mitatu ya uongozi wa serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan, kwa upande wetu mkoa wa Manyara, tumepiga hatua kubwa atika sekta ya afya," amesema Sendiga.

Amesema mara baada ya tukio hilo wagonjwa na majeruhi wa maafa hayo walipatiwa matibabu kwenye hospitali ya wilaya ya Hanang' (Tumaini).

Amesema wagonjwa na majeruhi wengine walipatiwa rufaa kwenye hospitali ya mkoa wa Manyara iliyopo mjini Babati hivyo hawakutoka nje ya Manyara.

"Wataalamu wa tiba tuu wakiwemo madaktari bingwa ndiyo walitoka nje ya Manyara, ila kwa upande wa dawa na vifaa tiba tupo vizuri, ndiyo sababu wagonjwa na majeruhi wote walitibiwa hapa kwetu," amesema Sendiga.

Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Hanang' Rose Kamili amemshukuru mkuu huyo wa mkoa kwa namna alivyoshiriki ipasavyo katika maafa hayo.

"Tunakushukuru wewe na viongozi wengine wa mkoa huu na wilaya nyingine kwa namna mlivyotukumbatia mara baada ya sisi kupatwa na maafa hayo yaliyoondoka na wapendwa wetu," amesema Kamili.


Na. Mwandishi wetu, Mwanza

Kamati ya kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii imempongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuridhia Mfuko wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) kuendeleza ujenzi wa kitega uchumi ambacho ni Hoteli yenye hadhi ya nyota Tano jijini Mwanza (Mwanza Tourist Hotel) ambao ulisimama kwa takribani miaka nane.

Akizungumza Machi 18, 2024 Mwenyekiti wa kamati hiyo Mhe. Fatma Toufiq, amesema ujenzi huo ukikamilika utachochea ukuaji wa uchumi na maendeleo ya mkoa wa Mwanza na Taifa kwa ujumla.

Awali, akisoma taarifa ya utekelezaji wa mradi huo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Prof. Joyce Ndalichako amesema mradi huo unatarajiwa kukamilika mwezi Desemba Mwaka huu na utazalisha ajira zaidi ya 250.

Kwa upande wake, Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Patrobas Katambi amesema Hoteli hiyo inajengwa kwa kuzingatia viwango vya kimataifa na itakuwa na uwezo wa kuhudumia wageni kutoka Mataifa mbalimbali.

Naye, Mkurugenzi Mkuu wa NSSF, Masha Mshomba ameihakikishia kamati hiyo kuendelea kusimamia ujenzi wa Hoteli hiyo ili ukamilike kwa wakati.






Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. George Simbachawene akiongea na maafisa uchunguzi wa Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma katika kikao kazi cha wachunguzi Kilichofanyika katika ukumbi wa Ngorongoro jijini Arusha tarehe 18 Machi 2024.
Kamishna wa Maadili, Jaji (Mst.) Sivangilwa Sikalalilwa Mwangesi akiongea na maafisa uchunguzi wa Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma katika kikao kazi cha wachunguzi Kilichofanyika katika ukumbi wa Ngorongoro jijini Arusha tarehe 18 Machi 2024.

..........

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi na Utawala Bora, Mhe. George Simbachawene (Mb) ametoa wito kwa watumishi wa Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Umma kutoka ofisini kwenda kwa wananchi kusikiliza malalamiko yao na kuyatafutia ufumbuzi badala ya kukaa ofisini kusubiri wananchi wachache wanaolalamikia viongozi.

“Sekretarieti ya Maadili nendeni mkawasilikize wananchi, yapo mambo wanayapigia kelele sana kuhusu tabia na mwenendo wa viongozi wao. Kelele zao zinaposikika tokeni mkawasikilize, hii itasaidia kutatua kero zao na mtawasaidia pia viongozi kujirudi na kufuata misingi ya maadii,” alisema.

”Tusichelewe sana kushughulikia malalamiko yanayotolewa na wananchi hadhalani.”

Mhe. Simbachawene alisema hayo jijini Arusha tarehe 18 Machi, 2024 wakatiakifungua kikao kazi cha Wachunguzi wa Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadii ya Viongozi wa Umma.

“Misingi hii lazima tuilinde na hili ndilo jukumu letu. Misingi hii isipozingatiwa, wananchi wanakosa huduma na malengo ya nchi hayatafikiwa,” alisema.



Kwa mujibu wa Mhe. Waziri, lazima watumishi wa Sekretarieti ya Maadili watoe elimu kuhusu misingi ya maadli na kusikiliza changamoto zao.

Katika hatua nyingine Mhe. Simbachawene alisema jukumu la kusimamia maadili linahitaji mtumishi anayetumia mbinu, busara na weledi wa hali ya juu kutokana na kuwahusu viongozi wakubwa na ni la kikatiba.

“Maadili ni zaidi ya sheria, lazima msimamie maadili ya viongozi wote kuanzia ngazi ya chini. Twende mbali tuanzie ngazi ya chini huko serikali za mitaa kusimamia maadili. Tusihangaike na viongozi wanaojaza fomu za Tamko tu kwasababu lazima kiongozi yeyote lazima awe mwadilifu,” alisema na kuongeza kuwa, “maadili katika jamii zetu ni jambo la msingi na lilikuwepo hata wakati wa ujima.”

Awali akimkaribisha Mhe. Waziri, Kamishna wa Maadili Mhe. Jaji (Mst.) Sivangilwa Mwangesi alieleza kuwa Taasisi imeona umuhimu wa wachunguzi wote kuwa na kikao cha pamoja kujadili mustakabali wa majukumu yao.

“Hii ni mara yetu ya kwanza tangu Taasisi ilipoanzishwa mwaka 1996 kuwa na kikao kama hiki kwa lengo la kuwakutanisha wachunguzi wote ndani ya Taasisi kujadili kwa kina mambo mbalimbali yanayohusu utendaji wa kazi na mafanikio kwa mujibu wa matakwa ya Ibara ya 132 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977,” alisema.

Kwa mujibu wa kifungu cha 19(2) cha Sheria ya Maadili ya Viongizo wa Umma Na. 13 ya 1995, majukumu ya Sekretarieti ya Maadili ni kupokea malalamiko ya ukiukwaji wa maadili, kufanya uchunguzi, kupokea matamko, kufanya uhakiki na kutoa elimu ya maadili.

Majukumu mengine ni kufanya utafiti wa hali ya uadilifu nchini, kutoa ushauri katika mambo ya uadilifu na kubuni mikakti ya ukuzaji maadili.

Mhe. Sivangilwa alizitaja mada zitakazo wasilishwa kuwa ni; Utendaji katika Ofisi za Kanda, Viambata vya Makosa ya Maadili, Utaratibu wa zoezi la Uhakiki, Mikakati ya utendaji kazi pamoja na Changamoto na utatuzi wake katika kushughulikia malalamiko na uchunguzi.



Na Benny Mwaipaja, Dodoma

WAZIRI wa Fedha, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb), ameishukuru Denmark kwa kuchangia maendeleo ya Tanzania katika nyanja mbalimbali za kiuchumi na kijamii pamoja na ujenzi wa mradi wa Reli ya Kisasa (SGR) kipande cha Morogoro hadi Makutupora mkoani Singida.

Dkt. Nchemba ameyasema hayo alipokutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Denmark nchini Tanzania, Mheshimiwa Mette Dissing-Spandet, Ofisini kwake Jijini Dodoma ambapo walijadili masuala kadhaa ya ushirikiano.

Alisema kuwa uhusiano wa Tanzania na Denmark umetimiza miaka 60 na katika kipindi hicho nchi hizo mbili zimekuwa na uhusiano mzuri wa kidiplomasia na kiuchumi ambapo hivi karibuni nchi hizo zilikuwa zikitekeleza miradi ambayo Denmark iliipatia Tanzania msaada wa takriban Denish Krone bilioni 2, sawa na shilingi za Tanzania bilioni 646.

Aidha, Dkt. Nchemba alisema kuwa Denmark kupitia Shirika ake la Maendeleo (DANIDA), imetoa zaidi ya shilingi bilioni 103 zinazotokana na mapato ya uwekezaji wake wa hisa katika Benki ya CRDB, ambazo zimetumika kwa ajili ya kusaidia sekta ya afya kupitia Mfuko wa Afya.

Aidha, aliipongeza Denmark kwa kusitisha uamuzi wake wa kutaka kufunga Ubalozi wake hapa nchini na kwamba hatua hiyo itaimarisha zaidi ushirikiano kwa manufaa ya wananchi wa pande hizo mbili.

Dkt. Nchemba alisema kuwa Tanzania iko tayari kushirikiana na Denmark kupitia mpango wake mpya wa ushirikiano baada ya kusitisha uamuzi huo wa kufunga ubalozi wake nchini ambapo nchi hiyo imepanga kuongeza kiwango cha ufadhili na kuelekeza fedha hizo kwenye maeneo yatakayokuza uchumi, ikiwemo nishati, kuboresha mifuko ya kodi, kilimo, elimu, afya, pamoja na kusaidia sekta binafsi.

Dkt. Nchemba pia alitumia fursa hiyo kuwakaribisha wawekezaji kutoka Denmark kuja kuwekeza mitaji yao hapa nchini ikiwemo sekta ya fedha na kunufaika na vivutio vilivyowekwa na Serikali baada ya kurekebisha sheria kadhaa, lakini pia kunufaika na soko la uhakika linalopatikana katika nchi za SADC na Jumuiya ya Afrika Mashariki.


Aliiomba pia Denmark kupitia Taasisi yake inayohusika na masuala ya Bima na Dhamana (Danish Export Credit Agency), kushiriki katika ujenzi wa mradi wa SGR kwa vipande vilivyobaki kutokana na umuhimu wa mradi huo katika kukuza biashara na ustawi wa maisha ya watu watakao tumia reli hiyo pamoja na kukuza pato la Taifa.

Kwa upande wake, Balozi wa Denmark nchini Tanzania, Mheshimiwa Mette Dissing-Spandet alisema kuwa nchi yake inapongeza mafanikio makubwa ya kiuchumi na kijamii yanayoendelea hivi sasa na kwamba iko tayari kutoa ushirikiano unaohitajika ili kuimarisha zaidi uhusiano wa nchi hizo mbili.
Mheshimiwa Spandet alisema kuwa nchi yake iko tayari kushirikiana na Tanzania katika eneo la nishati jadidifu, pamoja na gesi na kusaidia kukuza sekta binafsi ili iweze kuchangia maendeleo ya nchi.

Alisema kuwa Waziri wa Ushirikiano wa Maendeleo Kimataifa, Mhe. Dan Jorgensen, anatarajia kufanya ziara rasmi ya kikazi hapa nchini mwanzoni mwa mwezi Aprili mwaka huu, ambapo atatumia ziara hiyo kujadiliana na Serikali maeneo ya kipaumbele ambayo nchi hizo zitajielekeza katika mpango huo mpya wa ushirikiano.
Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb), akizungumza wakati wa Mkutano na Balozi wa Denmark hapa nchini, Mhe. Mette Dissing-Spandet, ambapo ameishukuru nchi hiyo kwa kuchangia maendeleo ya Tanzania katika nyanja mbalimbali za kiuchumi na kijamii pamoja na ujenzi wa mradi wa Reli ya Kisasa (SGR) kipande cha Morogoro hadi Makutupora mkoani Singida. Mkutano huo umefanyika Katika Ukumbi wa Mikutano wa Waziri wa Fedha, Jijini Dodoma.
Balozi wa Denmark nchini Tanzania, Mhe. Mette Dissing-Spandet, akizungumza wakati wa Mkutano wake na Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb), ambapo alisema kuwa nchi yake iko tayari kushirikiana na Tanzania katika eneo la nishati jadidifu, pamoja na gesi na kusaidia kukuza sekta binafsi ili iweze kuchangia maendeleo ya nchi. Mkutano huo umefanyika Katika Ukumbi wa Mikutano wa Waziri wa Fedha, Jijini Dodoma.
Ujumbe wa Tanzania ukiongozwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb) (wa pili kulia), ukiwa katika Mkutano na Ujumbe kutoka Ubalozi wa Denmark nchini, ukiongozwa na Balozi wake, Mhe. Mette Dissing-Spandet, mkutano uliofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Waziri wa Fedha, Jijini Dodoma.
Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb) (kulia), akiagana na Balozi wa Denmark hapa nchini, Mhe. Mette Dissing-Spandet, baada ya Mkutano wao uliofanyika Katika Ukumbi wa Mikutano wa Waziri wa Fedha, Jijini Dodoma. Katika Mkutano huo Mhe. Dkt. Nchemba, aliishukuru nchi hiyo kwa kuchangia maendeleo ya Tanzania katika nyanja mbalimbali za kiuchumi na kijamii pamoja na ujenzi wa mradi wa Reli ya Kisasa (SGR) kipande cha Morogoro hadi Makutupora mkoani Singida.
Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb) (katikati), akifurahia jambo na Balozi wa Denmark hapa nchini, Mhe. Mette Dissing-Spandet (kushoto) na Mkuu wa masuala ya Biashara wa Ubalozi wa Denmark nchini Tanzania, Bw. Oscar Mkude, baada ya Mkutano wao uliofanyika Katika Ukumbi wa Mikutano wa Waziri wa Fedha, Jijini Dodoma.
Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb) (katikati) na Balozi wa Denmark hapa nchini, Mhe. Mette Dissing-Spandet (wa nne kushoto) wakiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Viongozi wa Wizara ya Fedha na Mkuu wa masuala ya Biashara-Ubalozi wa Denmark nchini Tanzania, Bw. Oscar Mkude (wa nne kulia) baada ya kufanya mazungumzo yao, ambapo Dkt. Nchemba, ameishukuru nchi hiyo kwa kuchangia maendeleo ya Tanzania katika nyanja mbalimbali za kiuchumi na kijamii pamoja na ujenzi wa mradi wa Reli ya Kisasa (SGR) kipande cha Morogoro hadi Makutupora mkoani Singida. Mkutano huo umefanyika Katika Ukumbi wa Mikutano wa Waziri wa Fedha, Jijini Dodoma.


(Picha na Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali, WF, Dodoma)

Top News