Na Mwandishi wetu,Tunduru

WAKULIMA wa zao la korosho wa mikoa ya Mbeya,Njombe na Ruvuma wanaohudumiwa na Chama kikuu cha Ushirika wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma(Tamcu),wamevuka lengo la uzalishaji wa zao hilo katika msimu wa kilimo 2023/2024.

Ni baada ya kufanikiwa kuzalisha na kuuza jumla ya  tani elfu 26.066 sawa na kilo milioni 26,066,333 zenye thamani ya Sh.bilioni 45,531,514,557 sawa na ongezeko la tani 1,000 ikilinganisha na msimu uliopita ambapo walizalisha kiasi cha  tani 25,000.

Kaimu meneja wa Tamcu Marcelino Mrope amesema hayo jana,wakati akizungumza na wanachama wa chama cha msingi cha  Ushirika Ligunga(Ligunga Amcos) katika mnada wa nane na wa mwisho katika msimu wa kilimo 2023/2024.

Mrope alisema,hayo ni mafanikio makubwa kwa wakulima na Chama hicho katika uzalishaji wa korosho  ambapo amewapongeza wakulima kwa kazi nzuri waliyoifanya mashambani kwa mwaka 2023/2024.

Ameishukuru serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kutoa pembejeo za kilimo bure kwa wakulima, hali iliyohamasisha wakulima wengi kurudi mashambani kwa ajili ya kufufua mashamba yao.

“kwa mfano katika msimu huu wa kilimo 2024/2025 tumepewa pembejeo zenye thamani ya Sh.bilioni 22.5 kitu ambacho hakijawahi kutokea tangu nchi ipate Uhuru,tunaamini pembejeo hizi zitakwenda kuongeza sana uzalishaji wa korosho katika wilaya yetu”alisema Mrope.

Amewashauri wakulima kutumia  vizuri fedha walizopata kununua pembejeo na kutumia mvua zilizoanza kunyesha kuanza maandalizi ya msimu mpya wa kilimo 2024/2025.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa TAMCU Mussa Manjaule alisema,bei ya korosho  katika msimu wa mwaka huu haikuwa nzuri ikilinganisha na msimu uliopita,hata hivyo amewataka wakulima kutokatishwa tamaa badala yake waendelee kulima zao hilo ambalo ni nguzo kuu ya uchumi wao na wilaya  ya Tunduru.

Manjaule,ametoa ushauri wake kwa wakulima kuanza kulima mazao mengine ya chakula na biashara ikiwemo zao maarufu la mbaazi ambalo lina soko la uhakika na bei kubwa  na halihitaji gharama kubwa katika uzalishaji wake.

Naye afisa ushirika wa wilaya hiyo Georg Bissan,ameipongeza bodi ya chama kikuu cha ushirika(Tamcu) kwa kusimamia vyema mauzo ya korosho kwa mfumo wa stakabadhi ghalani ambao umewezesha wakulima kuwa na soko la uhakika na kupata fedha zao kwa wakati.

Amewaasa wakulima kutumia fedha walizopata kufanya mambo ya maendeleo ikiwemo ujenzi wa nyumba bora,kusomesha watoto na kuanzisha shughuli nyingine zitakazowaingizia kipato badala ya kutumia fedha hizo kwenye ulevi na uesharati.

Rashid Millanzi mkulima wa korosho,ameipongeza serikali kupitia chama kikuu cha ushirika(Tamcu) kuimarisha mfumo wa stakabadhi ghalani,hata hivyo ameiomba kutafuta wafanyabiasha wengi watakaokwenda kununua korosho kwa bei nzuri inayolingana na gharama za uzalishaji wake.

Wawakilishi wa wakulima wa korosho kutoka chama cha msingi cha ushirika cha Ligunga wilayani Tunduru,wakiangalia bei ya korosho  kutoka kwa wanunuzi wa zao hilo walioomba kununua korosho katika mnada wa  8 na wa mwisho kwa msimu wa kilimo 2023/2024,kulia meneja shughuli wa Chama kikuu cha ushirika wilayani Tunduru(Tamcu Ltd)Marcelino Mrope.
Baadhi ya wananchi wa kijiji cha Ligunga wilayani Tunduru,wakifuatilia uendeshaji wa mnada wa zao la korosho uliofanyika leo(jana) katika chama cha msingi cha ushirika Ligunga ambapo zaidi ya kilo 650,000 ziliuzwa katika mnada huo ambao ni wa mwisho kufanyika  wilayani humo.
Mwenyekiti wa Chama kikuu cha Ushirika wilayani Tunduru(Tamcu Ltd)Mussa Manjaule akizungumza na wakulima wa korosho wa kijiji cha Ligunga(hawapo pichani) baada ya kukamilika kwa mnada wa  8 na wa mwisho wa ununuzi wa zao la korosho kupitia mfumo wa stakabadhi ghalani kwa msimu wa kilimo 2023/2024 ambapo jumla ya kilo milioni 26,066,333 za korosho zenye thamani ya Sh.bilioni 45 zimezalishwa na kuuzwa.
 

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...