Marehemu Komando wa vikosi maalum Luteni Rajabu Mlima
Marehemu Komando Luteni Rajabu Mlima akipokea tuzo enzi za uhai wake
Ilipotimu safari,kamanda yupo tayari
Tena kwenye msitari,kutekeleza amri
Hakukifanya kiburi,Kusema ninasubiri
Mungu akulazepema kamanda Rajabu Mlima
Uliifanya safari,Niyako wewe hiyari
Ulifahamu hatari,zaweza kukukabiri
Molla atakusitiri,kuufanya ujasiri
Mungu akulazepema kamanda Rajabu Mlima
Tulijiweka tayari,kwahamu kukusubiri
Urejeapo safari,utapikiwa futari
Bakulini na mtori,upate kujisitiri
Mungu akulazepema kamanda Rajabu Mlima
Kifo hakina hiyari,Huwezi ukatabiri
Hakiwezi kusubiri,Imepitishwa amri
Linakuaga kaburi,hiyo ndiyo yake siri
Mungu akulazepema kamanda Rajabu Mlima
Siri ndiyo siri,Haitakuwa dhahiri
Japo uwe mashuhuri,maiti hawi jasiri
Huna tena ufahari,Nyumba yako nikaburi
Mungu akulazepema kamanda Rajabu Mlima
Kaburi imekua siri,masikini na tajiri
Hatuna yetu hiyari umekatiwa shauri
Mimi ninafikiri,Nasubiri hiyari
Mungu akulazepema kamanda Rajabu Mlima
Mitatu imedhihiri,Ndani yalako kaburi
Allah amekukiri,Usijekua kiburi
Hujafanya ufedhuri,Hili jambo si fahari
Mungu akulazepema kamanda Rajabu Mlima
Uhai tutafakari,Hakuna aliye hatari
Hii ni yake kahari,Asokuwa namshauri
Tena niyake fahari,Chumvi iwe sukari
Mungu akulazepema kamanda Rajabu Mlima
Mazuri huwa mazuri yasipopata dosari
Kuchota kwenye buri Siyosawa nabahari
Lazima tutafakari mja hana hiyari
Mungu akulazepema kamanda Rajabu Mlima
Nakiri nikisubiri zamu yangu ndiyo siri
Haina chakutabiri,ninasubiri kaburi
Siku itapo dhihiri,Sitakua jasiri
Mungu akulazepema kamanda Rajabu Mlima
Rabbi atusitiri, Ndani yahilo kaburi
Usipate ufakiri,mazuri nayawe mazuri
Kwenye lako daftari yaandikwe yaso shari
Mungu akulazepema kamanda Rajabu Mlima
MTUNZI: WAKO MAMA TUNGURI RAJABU TAMBWE
MOLA MLAZE PEMA PEPONI. (MAREHEMU LUTENI RAJABU MLIMA).
ReplyDeleteBismilahi nianze, kuwapa Pole wafiwa,
Kilio na tunyamaze, umauti meumbiwa,
Popote na tujibanze, 'Ziraili' tufichuwa,
YARABI mlaze pema, LUTENI RAJABU MALIMA.
Pema RABI amlaze, dhambize kusamehewa,
Nuruye amuangaze, adhabuze kumvuwa,
Jannatuye amwingize, siku ya kuhukumiwa
YARABI mlaze pema, LUTENI RAJABU MALIMA.
Kifo katu si khiyari, kila mtu kapangiwa,
Katu hakina tajiri, mali zao wangetowa,
'Munkari Wa Nakiri', kwa sote twasubiriwa,
YARABI mlaze pema, LUTENI RAJABU MALIMA.
Kifo hakina miadi, taarifa katu towa,
Hakina kupiga hodi, seuze kikachaguwa,
Katu wa kukikaidi, ni kuja na kuchukuwa,
YARABI mlaze pema, LUTENI RAJABU MALIMA.
Kifo hakionekani, suraye tukaijuwa,
Zoeleka abadani, maarufu tunajuwa,
Yote ni ya MOLA shani, kuumba na kuumbuwa,
YARABI mlaze pema, LUTENI RAJABU MALIMA.
Tujaliye mwisho mwema, ILAHI twaomba duwa
Utupe safi kalima, SHAHADA tuje tambuwa,
'Saqaratu' la salama, kila mja barikiwa,
YARABI mlaze pema, LUTENI RAJABU MALIMA.
Inna Lillahi Wainna Ilayhi Rajiun. Mwenyeez Mungu Mlaze Pema Peponi Marehemu LUTENI RAJABU MALIMA. AMEN.
mungu amlaze pema inshaallah..inaumiza sana lkn ndio hivyo Mungu alimchagua....
ReplyDeleteWahusika samahanini sana, tafadhalini sana naomba mniwie radhi, nilighafilika nikataamaki nImeandika MALIMA badala ya jina sahihi la 'MLIMA'. Samahani kwa kosa hilo la kiuandishi.
ReplyDelete