Na Jacquiline Mrisho – MAELEZO.
Chuo
Kikuu cha Ardhi kimetoa zawadi na tuzo kwa wanafunzi 104 waliofanya
vizuri kitaaluma ili kutoa hamasa kwa wanafunzi wengine kuweka juhudi
katika masomo.
Zawadi hizo zimetolewa leo
Jijini Dar es Salaam na Makamu Mkuu wa Chuo hicho, Prof. Idrissa Mshoro
ambaye ametangaza kuwa jumla ya wanafunzi wanne kati ya waliofanya
vizuri wamepata alama sawa hivyo kuibuka washindi wa jumla kwa mwaka
2016.
Akisoma hotuba wakati wa sherehe hizo,
Kaimu Naibu Makamu Mkuu wa Chuo hicho (Taaluma), Prof. Gabriel Kassenga
amesema kuwa sherehe hizo zimekuwa zikiwezeshwa na wadau mbalimbali
waliojitoa kwa hali na mali kutoa zawadi na tuzo kwa wanafunzi
waliofaulu vizuri kwenye vipengele mbalimbali vya taaluma hivyo
amewasihi wadau hao kuendelee kuunga mkono jitihada zinazofanywa na
wanafunzi hao ili kuwashawishi wanafunzi wengine kufanya vizuri.
“Zawadi
mbalimbali zinazotolewa na wafadhili zimekua zikiwasaidia wanafunzi
hawa kuongeza tija kwenye maisha yao ya kielimu na kiuchumi kwani wengi
wao wamekuwa wakizitumia fedha hizo kama mitaji ya kufanyia biashara
pindi wamalizapo masomo yao,”alisema Prof. Kassenga.
Amefafanua
kuwa mwaka huu umekuwa wa tofauti kwani idadi ya wanafunzi wanawake na
wanaume waliopata tuzo hizo iko sawa tofauti na miaka mitatu iliyopita
ambapo wanawake walikua wakiongoza kwa asilimia 3.7 kwa kupata tuzo
nyingi wakati wanaume wakiwa ni asilimia 2.2.
Prof.
Kassenga ametaja baadhi ya zawadi zilizotolewa na wafadhili
walioshiriki katika shughuli hiyo kuwa ni vyeti, Kompyuta mpakato
(laptop),vifaa vinavyotumika katika kupimaji wa ardhi pamoja na fedha
taslimu.Aidha, Prof. Kassenga ametoa rai kwa
kwa wanafunzi wote waliomaliza chuoni hapo kuwa juhudi walizokuwa
wakizionyesha wakati wa masomo waende wakaziendeleze katika jamii
zinazowazunguka pamoja na kwenye shughuli mbalimbali za ujenzi wa Taifa
ili wakawe mfano bora kwa vizazi vijavyo.
Kwa upande wake
Emily Elandogo ambaye ni mmoja kati ya wanafunzi waliopewa zawadi hizo
amewashukuru walimu wa chuo hicho kwa elimu wanayoitoa ambayo itakua ni
chanzo cha kuwaletea maendeleo sehemu yoyote watakapokuwa pia ametoa
ushauri kwa wanafunzi wenzake kuitumia vizuri elimu waliyoipata ili
iweze kuwasaidia katika maisha yao.
Mahafali
ya Kumi ya chuo hicho yanategemewa kufanyika Disemba 3 mwaka huu katika
viwanja va chuo hicho ambapo wahitimu wa shahada mbalimbali
watatunukiwa stahili pamoja na vyeti vyao.
Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Ardhi, Prof. Idrissa Mshoro (katikati kulia) akiteta jambo na Kaimu Naibu Makamu Mkuu wa Chuo hicho (Taaluma), Prof. Gabriel Kassenga(katikati kushoto), pembeni kulia ni Kaimu Naibu Makamu Mkuu wa chuo hicho (Mipango, Fedha na Utawala),Prof. Robert Kiunsi, pembeni kushoto ni Maafisa Waandamizi wa chuo hicho. Shughuli hizo zimefanyika leo Jijini Dar es Salaam katika viwanja vya chuo hicho.
Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Ardhi, Prof. Idrissa Mshoro akiwa katika picha ya pamoja na watumishi wa chuo na wanafunzi waliofanya vizuri kitaaluma wakati wa shughuli za ugawaji wa vyeti na zawadi kwa wanafunzi waliofaulu masomo mbalimbali uliofanyika leo Jijini Dar es Salaam katika viwanja vya chuo hicho.
Mmoja kati ya washindi wa jumla wenye alama za juu, Anyighwile Lwijiso akipokea zawadi kutoka kwa mmoja wa wafadhili ambao ni Kampuni ya Hightech System mara baada ya kutangazwa kuwa mshindi. Shughuli hizo zimefanyika leo Jijini Dar es Salaam katika viwanja vya chuo hicho.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...