RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa
Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameeleza kuwa azma ya Benki ya NMB ya
kuendelea kuziunga mkono juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika
kuimarisha miradi ya maendeleo katika jamii itasaidia kuimarisha uchumi na
kuleta tija kwa wananchi wa Zanzibar.
Dk. Shein aliyasema hayo
alipozungumza na Mkurugenzi Mkuu wa Benki ya NMB nchini Tanzania Bi Ineke
Bussemaker alipofika Ikulu mjini Zanzibar. Katika maelezo yake, Dk. Shein
alisema kuwa Benki ya NMB imekuwa na mchango mkubwa katika kuzisaidia sekta za
maendeleo hapa nchini zikiwemo sekta ya afya, elimu na nyinginezo hatua ambayo
ni muhimu katika kufikia malengo yaliyokusudiwa.
Aidha, Dk. Shein aliipongeza Benki
hiyo kwa kuanzisha programu mbali mbali za kuwasaidia wakulima wakiwemo wa zao
la karafuu hapa nchini na kueleza lengo la Serikali ni kuona zao la karafuu
linaimarika na ndio maana imekuwa ikichukua juhudi za makusudi ili kuhakikisha
zao hilo linapata sifa kimataifa. Sambamba na hayo, Dk. Shein alimuhakikishia
Mkurugenzi huyo kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kushirikiana
na Benki hiyo katika kuimarisha sekta za maendeleo na kukuza uchumi wa nchi na
wananchi wake.
Naye Mkurugenzi Mkuu wa NMB Tanzania,
Bi Ineke Bussemaker alipongeza juhudi zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi
ya Zanzibar katika kuimarisha miradi ya maendeleo katika jamii na kuahidi
kuendelea kuunga mkono.
“Benki ya NMB imeweza kushirikiana
na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika miradi kadhaa ikiwemo miradi ya
elimu kwa kusaidia madawati, afya, kilimo na
tunaahidi kuendeleza miradi hii kwa lengo la kuinua kipato cha mwananchi
wa Zanzibar. Pia tunaendelea na azma yetu ya kusaidia kompyuta 50 kwa skuli za
Zanzibar ” aliongeza Bi Bussemaker
Pia, Mkurugenzi huyo alieleza hatua
zinazoendelea kuchukuliwa na Benki yake katika mradi wa kuwasaidia wakulima
katika kuimarisha na kusafirisha bidhaa zao zikiwemo bidhaa za viungo na
kusisitiza umuhimu wa kukusanya mapato kwa kutumia mfumo wa kisasa wa “e-tax”
ambapo benki yake tayari imeshaanza mchakato huo kwa upande wa Tanzania Bara.
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein akiwa katika mazungumzo na Mkurugenzi Mkuu wa Benki ya NMB nchini Tanzania Bi Ineke Bussemaker alipofika Ikulu mjini Zanzibar.
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein akiwa katika picha ya pamoja baada ya mazungumzo na Mkurugenzi Mkuu wa Benki ya NMB nchini Tanzania Bi Ineke Bussemaker na ujumbe wake walipofika Ikulu mjini Zanzibar.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...