Na Veronica Simba.

Serikali imesema itaifungia migodi yote ya madini ambayo itapata ajali kutokana na uzembe na haitafunguliwa hadi hapo Mkaguzi Mkuu wa Migodi atakapojiridhisha kuwa hali ya usalama imeboreshwa na hatua stahiki za kisheria zimechukuliwa kwa Meneja wa Mgodi au Msimamizi aliyehusika na uzembe huo.

Hayo yalisemwa hivi karibuni na Kamishna wa Madini Tanzania, Mhandisi Benjamin Mchwampaka wakati akifungua mafunzo maalum kwa wachimbaji wadogo wa madini nchini, kwa lengo la kuwakumbusha kuzingatia kanuni zote za usalama mahali pa kazi ili kuepusha ajali za mara kwa mara zinazotokea na kusababisha vifo.

Mafunzo hayo ambayo yameandaliwa na Wizara ya Nishati na Madini, kupitia Idara yake ya Madini, yalifunguliwa rasmi Mererani, wilayani Simanjiro, Mkoa wa Manyara, ambapo Kamishna Mchwampaka aliwaambia wachimbaji wadogo wa madini wa eneo hilo kuwa, kwa sasa uchimbaji mdogo wa madini nchini umegubikwa na ajali nyingi ambazo zinaweza kuepukika endapo tahadhari za kiusalama zitachukuliwa.

“Ajali zinazotokea katika Migodi mingi ya wachimbaji wadogo hapa nchini, zimesababisha vifo, vilema vya maisha na pia gharama kubwa wakati wa shughuli za uokoaji.”

Kamishna Mchwampaka alisema kuwa, Serikali imelazimika kuchukua hatua za makusudi kuhakikisha kuwa uchimbaji madini nchini, unafanyika kwa mujibu wa Sheria ya Madini kwa kuzingatia usalama na pia utunzaji wa mazingira.
 Kamishna wa Madini Tanzania, Mhandisi Benjamin Mchwampaka (wa pili kutoka kulia), akijibu maswali mbalimbali kutoka kwa wachimbaji wadogo wa madini wa eneo la Mererani, wakati wa mafunzo maalum kuhusu usalama migodini yaliyofanyika hivi karibuni. Wengine pichani (kutoka kulia) ni Mkaguzi Mkuu wa Migodi Tanzania, Mhandisi Ally Samaje, Kamishna Msaidizi wa Madini Kanda ya Kaskazini, Adam Juma na Fundi Sanifu Migodi kutoka Ofisi ya Madini Dar es Salaam, Stanslaus Basheka.
 Mkaguzi Mkuu wa Migodi Tanzania, Mhandisi Ally Samaje, akiwasilisha mada kuhusu Usalama, Afya na Utunzaji wa Mazingira katika Migodi ya Wachimbaji Wadogo wa Madini, wakati wa mafunzo maalum kwa wachimbaji wadogo wa eneo la Mererani yaliyozinduliwa rasmi hivi karibuni.
 Fundi Sanifu Migodi kutoka Ofisi ya Madini Dar es Salaam, Stanslaus Basheka, akiwasilisha mada kuhusu Matumizi salama na utunzaji wa baruti migodini, wakati wa mafunzo maalum kwa wachimbaji wadogo wa madini wa eneo la Mererani hivi karibuni.
 Ofisa wa Sheria kutoka Wizara ya Nishati na Madini, Hadija Ramadhan, akiwasilisha mada kuhusu Ufafanuzi wa Sera ya Madini ya Mwaka 2009, Ufafanuzi wa Sheria ya Madini ya Mwaka 2010 na Kanuni zake za Mwaka 2010, wakati wa mafunzo maalum kwa wachimbaji wadogo wa madini wa eneo la Mererani hivi karibuni.

HABARI ZAIDI BOFYA HAPA

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...