Na Rhoda James, DSM

Waziri wa Madini Angellah Kairuki mwishoni mwa wiki alikutana na Ujumbe wa Benki ya Dunia jijini Dar es Salaam kwa lengo la kufahamiana na kuangalia hatua mbalimbali zilizofikiwa katika utekelezaji wa Miradi ya Madini inayotekelezwa kupitia Mradi wa Usimamizi Endelevu wa Rasilimali Madini (SMMRP) unaofadhiliwa na Benki hiyo kwa kushirikiana na Serikali.

Pamoja na mambo mengine yaliyojadiliwa katika kikao hicho, Waziri Kairuki aliitaka Benki ya Dunia kuona namna ya kuwaendeleza Wataalam wa Sekta ya Madini ili kuwezesha uwepo wa Watalaam wa kutosha hususan katika masuala ya Uthaminishaji wa Madini ya Almasi, tanzanite na madini mengine ya vito na pia masuala ya uongezaji thamani madini kwa ujumla.

Pia, alishauri umuhimu wa kuboreshwa kwa Mtandao wa Huduma za Leseni kwa Njia ya Mtandao (Online Mining Cadastre) ikiwa ni pamoja na kuunganisha mtandao huo na Mamlaka nyingine ikiwemo Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na Wakala wa Jiolojia Tanzania (GST) ili taarifa zote zinazohusu madini na mapato yatokanayo na madini ziweze kupatikana kupitia mtandao huo.

Vilevile, aliishauri Benki hiyo kuhusu uuzwaji wa Madini ya Almas kwa njia ya Mnada kama vile inavyofanyika kwa Madini ya Tanzanite, lengo likiwa ni kuwezesha Serikali kunufaika na madini hayo. Aliongeza kuwa, baada ya Serikali ya Tanzania kupitisha Marekebisho ya Sheria ya Madini kupitia Sheria ijulikanayo kama (The written laws (Miscellaneous Amendements) Act, 2017), alisema kuwa, baadhi ya wawekezaji wameonesha wasiwasi kuhusu marekebisho hayo.

Hivyo, Waziri Kairuki amewataka wawekezaji kutokuwa na hofu kwani mabadiliko hayo yanalenga kuhakikisha kuwa Serikali inanufaika ipasavyo kutokana na rasilimali zake za madini. Aidha, alisema kwamba, nia ya Serikali kuhusu kuvutia wawekezaji iko palepale ilimradi wazingatie Sheria na taratibu. Vilevile, Waziri Kairuki alieleza kwamba, ni vema Benki ya Dunia ikaangalia namna bora ya kuhakikisha madini yote ya Tanzanite yanayouzwa nje ya nchi yanakuwa na Hati ya Uhalisia inayoonyesha chanzo cha madini hayo suala ambalo litawezesha Taifa kupata mapato stahiki kutokana na rasilimali hiyo.

Vievile, Waziri Kairuki alizungumzia suala la udhibiti wa utoroshaji madini na kusisitiza kuhusu kuwepo na namna bora ya kuzuia utoroshwaji wa madini ya Tanzanite ikiwemo kujulikana kwa idadi ya wachimbaji wadogo, wa kati, kiasi kinachopatikana na mahali madini hayo yanapouzwa. Pia, Waziri Kairuki aliishukuru Benki ya Dunia kutokana na ushirikiano ambao umekuwepo baina ya Serikali kwa kipindi chote na kueleza kuwa, Serikali iko tayari kutekeleza miradi husika kikamilifu kwa lengo la kukuza uchumi wa nchi.

BOFYA HAPA KUSOMA ZAIDI

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...