Na Zainab Nyamka,Globu ya Jamii.
BAADA ya kutokuwepo katika kikosi cha Yanga kwa muda mrefu, Mlinda mlango wa timu hiyo Beno Kakolanya ameweka wazi kuwa sasa amerejea baada ya kumalizana na uongozi kuhusu stahiki zake za fedha za usajili.
Kakolanya ambaye alijiunga na Yanga msimu wa 2016/17 kutokea Tanzania Prisons ya Mbeya baada ya kufanya vizuri kwenye msimu mzuri uliopita na kusaini kandarasi ya miaka miwili.
Takribani mwezi mmoja sasa Kakolanya amekuwa nje ya kikosi cha Yanga kukiwa na taarifa kuwa ana madai yake ya fedha za usajili na kushindwa kuungana na wenzake.
Akizungumza na Globu ya Michuzi, Kakolanya amesema kuwa tayari uongozi umemuhakikishia mwishoni mwa mwezi huu watamalizana nae fedha za usajili zilizosalia ila tayari ameanza kujumuika kwenye mazoezi na wenzake.
" Uongozi umeniambia kuwa mwishoni mwa mwezi huu watanipatia stahiki zangu kwahiyo kwa sasa naendelea na mazoezi kama kawaida nikiwa tayari nimeshaungana na wenzangu toka walivyorejea kutoka Zanzibar kwenye michuano ya Mapinduzi,"amesema Kakolanya.
Awali Kakolanya aliweka shinikizo la kutokuwepo katika kikosi cha Yanga hadi hapo atakapokamilishiwa fedha zake usajili ambazo alikuwa bado hajamaliziwa na uongozi wa klabu hiyo.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...