“Kesho ya Mtu hujengwa leo na Tofali la kujengea kesho hufyatuliwa leo” hii ni
kauli ya Sarah Kibonde Msika, Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na
Uhamasishaji kutoka Mamlaka ya Usimamizi wa Sekta ya Hifadhi ya Jamii – SSRA
akizungumza na vijana waliotembelea banda la Mamlaka hiyo kwenye Maonesho ya
13 ya Elimu ya Juu na Taasisi za Kitafiti na wadau wa elimu ya juu yanayoendelea
katika viwanja vya Mnazi Mmoja, jijini Dar es Salaam.
Akifanunua kauli hiyo, Mkuu huyo wa Kitengo kutoka SSRA anasema, Taifa
linakabiliwa na kiwango kikubwa cha umaskini wa kipato hasa kwa baadhi ya
makundi kama ya wazee, jambo linalotokana na watu wengi kutokuwa na utaratibu
wa kujiwekea akiba na maandalizi ya kufikia uzee, hivyo kuwahimiza vijana wenye
nafasi ya kurekebisha hali hiyo kuanza maandalizi mapema kwa kujiwekea akiba
kwa njia mbalimbali ikiwemo Mifumo ya Hifadhi ya Jamii .
Kwa kutambua changamoto hiyo ya umaskini wa kipato hasa wakati wa uzee, SSRA
inajukumu la kuhakikisha watanzania wanapata kinga kwa ajili ya kuwalinda dhidi ya
majanga ya kiuchumi na kijamii. Mpaka sasa imefanya juhudi ya kuanzisha mipango
ya kupambana na hali hiyo ikiwa ni pamoja na kuanzisha mfumo utakaoruhusu kila
kundi katika jamii kufaidika na huduma za Hifadhi ya Jamii. Miongoni mwa mipango
hiyo ni pamoja na mfumo wa hiari/ziada (Supplementary Schemes), wenye lengo la
kukabiliana na mahitaji mahususi ya nguvukazi katika sekta isiyo rasmi ambayo kwa
hakika inajumuisha sehemu kubwa zaidi ya nguvukazi nchini, anasema Sarah
Kibonde.
Akifafanua kuhusu Mpango huo, Sarah anasema chini ya usimamizi wa SSRA,
nguvukazi kutoka katika wa sekta isiyo rasmi na hata wanafunzi wa vyuo vikuu sasa
ina fursa ya kuchagua na kuchangia kiasi chochote wanachomudu kila mwezi au kila
mara kadiri watakavyoweza. Katika mfumo huo inahimizwa zaidi kuwa fao
litakalopatikana litategemea kiasi cha michango kitakachotolewa.
Kiasi cha
michango kinavyokuwa kikubwa zaidi ndivyo fao linavyokuwa kubwa zaidi. Kuhusu
utaratibu na namna ya kujiunga na mfumo huu wa hiari, Sarah anawashauri
vijana kutembelea katika ofisi za Mifuko yote ya Hifadhi ya Jamii.
Hivyo basi, SSRA inatumia maonesho haya ya Elimu ya Juu kuelimisha Umma juu
ya masuala ya Hifadhi ya Jamii hususani kukutana na vijana waliopo vyuoni na
wanaotarajiwa kuingia vyuoni, lengo likiwa ni kuwaelimisha na kuwaimiza kuweka
akiba jambo litakalowajengea tabia ya kuwekeza kwa ajili ya maisha ya baadae na
kuwaepusha na changamoto ya umaskini wa kipato wakati wa uzee. “Majuto ya
kesho huandaliwa leo” anasisitiza Bibi. Sarah Kibonde
Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na Uhamasishaji wa SSRA, Sarah Kibonde Msika akifafanua
jambo wakati kwa wadau waliotembelea banda la SSRA wakati wa Maonyesho ya Taasisi za Elimu
ya Juu yanaendelea katika Viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam.
Afisa Matekelezo wa SSRA, David Lyanga akitoa maelezo kwa wananchi waliotembelea banda la
SSRA lililoko kwenye Maonyesho ya Taasisi za Elimu ya Juu yanaendelea katika Viwanja vya Mnazi
Mmoja Jijini Dar es Salaam.
Baadhi ya wanafunzi wakiwa kwenye banda la SSRA wakati wa Maonyesho ya Taasisi za Elimu ya
Juu yanayoendelea katika viwanja vya Mnazi Mmoja jijni Dar es Salaam.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...