Na Shamimu Nyaki –WHUSM
Serikali imefikia hatua za mwisho za kukamilisha rasimu ya Sera ya Maendeleo ya Michezo baada ya kukusanya maoni kutoka kwa wadau ndani na nje ya nchi na ni matarajio ya wizara kukamilisha zoezi hili ndani ya muda mfupi.
Hayo yamesemwa leo Bungeni Jijini Dodoma na Waziri wa Habari Utamaduni Sanaa na Michezo Mheshimiwa Dkt. Harrison Mwakyembe alipokua akijibu swali la msingi la Mbunge Rashid Shangazi wa Mlalo (CCM) aliyeuliza kuwa ni lini serikali itakamilisha Sera ya Michezo.
“Zoezi la kupitia upya Sera ya Maendeleo ya Michezo ya mwaka 1995 ni zoezi ambalo limehusisha ukusanyaji wa maoni kutoka kwa wadau mbalimbali wa michezo na tayari rasimu kamili ya Sera hiyo imefikia hatua nzuri.”Alisema Dkt. Mwakyembe.
Aidha Mhe. Mwakyembe ameongeza kuwa Sera ya Michezo itakapokamilika itasaidia kuleta mabadiliko mengi ya kisera ikiwemo kuibuka kwa michezo ya kulipwa,mahitaji ya shule na vyuo mahususi vya michezo mbalimbali kwa lengo la kulea vipaji toka utotoni pamoja na uhitaji wa viwanja vizuri na vya kutosha ngazi za shule za msingi,sekondari, vyuo na sehemu za kazi.
Pamoja na hayo katika swali la nyongeza la Mbunge huyo wa Mlalo lililohoji kuhusu ushirikishwaji wa wabunge katika uandaaji wa Sera hiyo Waziri Mwakyembe alieleza kuwa wizara itaandaa utaratibu wa kuweza kuwashirikisha wabunge katika kutoa maoni yao.
Mheshimiwa Mwakyembe ameongeza kuwa Sera mpya itasaidia kuleta mabadiliko chanya katika tasnia ya michezo nchini ikiwa ni pamoja na kubadili sheria iliyoanzisha Baraza la Michezo la Taifa (BMT) ili iweze kuongeza ufanisi katika uendeshaji wa michezo nchini pamoja na kuanisha vyanzo rasmi vya mapato katika michezo.
Hata hivyo Waziri huyo mwenye dhamana na michezo nchini ametoa wito kwa Taasisi,Mashirika ya Umma,Vilabu na vyama vya michezo kutunza na kufanyia ukarabati viwanja vyote vinavyomiliki ili viwe na ubora unaotakiwa katika michezo
Waziri wa Habari Utamaduni Sanaa na Michezo Mhe. Dkt. Harrison Mwakyembe akizungumza leo Bungeni Jijini Dodoma.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...