Katika kuimarisha na kuboresha matibabu ya magonjwa ya moyo kwa watoto, Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) imeendelea kuboresha wodi ya watoto iliyopo katika jengo la watoto ili ifikapo Desemba mwaka huu wodi hiyo ianze kutoa huduma zote kwa watoto.

Wodi hiyo inatarajiwa kuwa na vitanda 32 ambapo vitanda nane vitakuwa katika chumba cha kulaza watoto wanaohitaji uangalizi maalum (ICU) na vitanda 24 katika wodi za kawaida za watoto, vyumba vitatu kwa ajili ya kliniki za watoto pamoja na vyumba kwa ajili ya ofisi .

Kwa kipindi cha miaka mitatu kuanzia 2015 hadi 2018 Taasisi imeona jumla ya watoto 8,000 wenye matatizo mbalimbali ya kuzaliwa nayo na yasiyo ya kuzaliwa nayo. Kwa upande wa upasuaji wa moyo jumla ya watoto 889 wamefanyiwa upasuaji wa moyo wa kufungua kifua na upasuaji wa bila kufungua kifua

Watoto 519 walifanyiwa upasuaji wa moyo wa kufungua kifua na kati ya hao watoto 238 walifanyiwa upasuaji na madaktari wetu bingwa wa magonjwa ya moyo huku watoto 281 walifanyiwa upasuaji wakati wa kambi maalum zilizowaunganisha madaktari wetu na madaktari kutoka shirika la Mending Kids International, SACH, na mashirika mengine. Upasuaji wa moyo wa bila kufungua kifua (Catheterization) kwa kutumia mtambo wa Cathlab ulifanyika kwa watoto 370

Kwa upande wa kliniki ya watoto kila siku inatoa huduma ya kati ya watoto 30 hadi 40 na kulaza mtoto mmoja hadi wawili. Tangu kuanza kwa mwaka huu wa 2018 jumla ya watoto 95 wamefanyiwa upasuaji wa kufungua kifua na bila kufungua kifua watoto 60

Zaidi ya asilimia 75 ya watoto wanaofanyiwa upasuaji ni wale wenye matatizo ya moyo ya kuzaliwa nayo ambayo ni matundu na magonjwa yanayoshambulia milango ya mishipa mikubwa na midogo ya moyo. Asilimia 25 ni wale ambao walizaliwa salama na kupata matatizo hayo baada ya kuzaliwa.
 
Imetolewa na:
Kitengo cha Uhusiano
Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete
18/10/2018.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...