Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa
amewataka wakazi wa mikoa ya Dodoma na Iringa kutumia fursa ya
kukamilika kwa kiwango cha lami barabara ya Dodoma Iringa kufanya
shughuli za uzalishaji ili kujiletea maendeleo.
Akizungumza wakati akikagua barabara ya Dodoma Iringa KM 260 Profesa
Mbarawa amesema Barabara hiyo imelenga kufufua uchumi wa mikoa ya
Iringa na Dodoma hususani hifadhi ya Ruaha na Vivutio vya utalii vilivyopo
mkoani Iringa.
“Barabara hii tuIiigawa katika sehemu tatu Iringa-Migori KM 95.2, Migori-
Fufu KM 93.8 na Fufu –Dodoma Km 70,9 ili ikamilike kwa haraka na hivyo
kuharakisha maendeleo ya watu wa Dodoma na Iringa “. Amesema
Profesa Mbarawa.
Profesa Mbarawa amesema kiasi cha sh. bil 4.6 itatolewa na Serikali ili
kulipa fidia kwa wananchi watakaopisha ujenzi wa barabara ya Iringa
mchepuo KM 7.3 itakayoanzia Kihesa –Kilolo kupitia Chuo Kikuu cha Iringa
hadi Igumbilo ili kuondoa msongamano wa magari katikati ya Mji wa Iringa.
Waziri Mbarawa amesisitiza nia ya Serikali ya kuukarabati uwanja wa
Ndege wa Nduli mkoani Iringa ili kuwawezesha watalii wanaokwenda
katika hifadhi ya Ruaha na Vivutio vingine vya Utalii Mkoani Iringa kutumia
uwanja huo ili kuhamasisha uchumi wa mkoa wa Iringa.
Naye Mbunge wa Isimani Mhe. Wiliam Lukuvi ambaye ni Waziri wa Ardhi,
Nyumba na Maendeleo ya Makazi akizungumza kwa niaba ya wabunge wa
Mkoa wa Iringa amemshukuru Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
Prof. Mbarawa kwa kukubali kujenga barabara ya Mchepuo ya Iringa na
kumuomba aangalie uwezekano wa kujenga kwa kiwango cha lami
barabara ya Iringa-Kalenga hadi katika hifadhi ya Taifa Ruaha yenye urefu
wa KM 104.
Mkuu wa Mkoa wa Iringa Bi. Amina Masenza amemuomba Waziri wa
Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kupanua barabara ya TANZAM eneo la
Mlima kitonga na kumalizia ujenzi wa barabara ya Tosamaganga
–Ugwachanya kwa kiwango cha lami na Ujenzi wa daraja la Tosamaganga
ili kupunguza changamoto za usafiri kwa wakazi wa Iringa.
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano yupo katika Ziara ya siku nne
mkoani Iringa kukagua maendeleo ya Ujenzi wa Miundombinu mkoani
humo.
Waziri Wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa
akimsikiliza Meneja wa wakala wa Barabara nchini (TANROADS) Mkoa wa
Iringa Eng. Daniel Kindole wakati wa ukaguzi wa barabara ya Dodoma
–Iringa KM 260 ambapo ujenzi wake umekamilika kwa kiwango cha lami.
Mkuu wa mkoa wa Iringa Bi. Amina Masenza akitoa taarifa ya hali ya
Miundombinu kwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa
Makame Mbarawa wakati wa ziara ya waziri huyo katika mkoani Iringa.
Waziri Wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa
akitoa maelekezo kwa watendaji wa taasisi zilizo chini ya Wizara ya Ujenzi,
Uchukuzi na Mawasiliano Mkoani Iringa. Kulia ni Waziri wa Ardhi Nyumba
na Maendeleo ya Makazi Mhe.William Lukuvi na Kushoto Mkuu wa mkoa
wa Iringa Bi Amina Masenza.
Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe.William Lukuvi
akifafanua jambo kwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa
Makame Mbarawa mara baada ya kuanza ziara ya siku nne mkoani Iringa.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...