Katika kuadhimisha Siku ya Sayansi Duniani, Kijiji cha Makumbusho Jijini Dar es Salaam kupitia Nyumba ya Wazaramo kimeunganisha nguvu za sayansi na jamii kwa lengo la kuonesha namna elimu ya sayansi inavyoweza kusaidia kuhifadhi urithi wa kitamaduni na kujenga jamii endelevu yenye amani.

Tukio hilo limewakutanisha wanasayansi, wahifadhi wa makumbusho, wanafunzi na jamii ya Wazaramo ili kusherehekea mchango wa sayansi katika maendeleo ya kijamii na kiutamaduni.

Akizungumza katika maadhimisho hayo leo Novemba 10, 2025, Mhifadhi Mwandamizi wa Makumbusho ya Taifa (NMT), Bi. Sechelela Magoile, amesema kaulimbiu ya mwaka huu inalenga kuhusisha sayansi na jamii kwa kuhakikisha wananchi wanapata taarifa sahihi kuhusu maendeleo ya kisayansi, kukuza uelewa na kuweka jamii salama.

Bi. Magoile ameeleza kuwa katika maadhimisho hayo, NMT imewasilisha utekelezaji wa mradi wa “Ukuaji wa Miji na Kupotea kwa Urithi wa Kitamaduni wa Jiji la Dar es Salaam” ambao unalenga kuonesha historia ya asili ya kabila la Wazaramo – wazawa wa eneo la Dar es Salaam – na jinsi maisha yao ya kila siku yanavyohusiana na sayansi katika nyanja za afya, uhifadhi wa chakula na mazingira.

“Tumeita wanafunzi ambao ndio umri sahihi wa kuelewa walipotoka na wanakoelekea katika utamaduni wao,” amesema Bi. Magoile.

Mradi huo unatekelezwa kwa ushirikiano kati ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Makumbusho ya Taifa, Chuo Kikuu cha SMUS Technische, na wanajamii kutoka jamii ya Wazaramo.

Kwa upande wake, Afisa Uratibu wa Utafiti kutoka Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH), Bw. Clavery Makoti, amesema ukuaji wa miji unaenda sambamba na maendeleo ya sayansi na teknolojia, hali ambayo inaweza kuwa na athari chanya au hasi kwa utamaduni wa jamii.

“Ni vyema tukajikita kufanya tafiti katika eneo hili ili kupata taarifa sahihi za kisayansi zitakazoainisha ukubwa wa upotevu wa utamaduni na namna bora ya kulitatua,” amesema Makoti.

Ameongeza kuwa COSTECH ingependa kuona ukuaji wa miji unaoenda sambamba na maendeleo ya sayansi na teknolojia yenye manufaa kwa utamaduni, si kwa jamii ya Dar es Salaam na Wazaramo pekee bali kwa makabila yote nchini.

“Tafiti za aina hii zitasaidia kuweka mizani kati ya maendeleo ya kisasa na uhifadhi wa urithi wa kitamaduni wa Tanzania,” amesisitiza.

Muandaaji wa Maonesho, Bw. Jackson Mwasha, amesema amekusanya taarifa kutoka kwa wadau mbalimbali ikiwemo jamii, wataalamu wa NMT na wanazuoni wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ili kufanikisha maandalizi ya maonesho hayo kwa dhima iliyokusudiwa.

Naye Bw. Mgeni Ramadhani Bway, mjenzi wa nyumba za asili za kabila la Wazaramo, amewashukuru Makumbusho ya Taifa kwa kuwashirikisha wananchi katika tafiti hizo, akisema hatua hiyo itasaidia vijana kujifunza na kuilinda jamii yao.

“Kushirikishwa kwetu ni fursa kubwa kwa vijana kujifunza na kuona umuhimu wa kulinda tamaduni zetu,” amesema Bway.

Kwa upande wake, Vainess Jofrey, mwanafunzi wa Shule ya Msingi Mbezi Ndumbwi, amesema kupitia maadhimisho hayo wamejifunza kuhusu utamaduni wa Kizaramo, ikiwemo maadili ya nidhamu, utii na ubunifu katika utengenezaji wa vifaa vya matumizi vinavyotokana na matawi ya mnazi.














Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Mhandisi Ramadhani Lwamo, amewataka watumishi wa Tume kujenga utamaduni wa kufanya mazoezi ya mwili mara kwa mara na kuepuka tabia zinazoweza kusababisha magonjwa sugu na maambukizi ya Virusi vya Ukimwi (VVU).

Mhandisi Lwamo ametoa wito huo Novemba 10, 2025, wakati akifungua mafunzo ya waelimisha rika wa Tume ya Madini yanayofanyika jijini Dodoma.

Amesema lengo la mafunzo hayo ni kuongeza uelewa miongoni mwa watumishi kuhusu VVU, Ukimwi na magonjwa yasiyoambukiza, ili kulinda afya zao na kuboresha ufanisi katika utekelezaji wa majukumu ya kila siku.

“Afya bora ya mwili na akili ni nguzo muhimu ya utendaji kazi wenye tija. Magonjwa mengi tunayokabiliana nayo leo yanatokana na mitindo ya maisha, ulaji usio sahihi, kutofanya mazoezi na tabia hatarishi za ngono. Ni jukumu letu kila mmoja kuhakikisha tunajilinda na kuishi kwa afya,” amesema Mhandisi Lwamo.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa waajiri kujumuisha mikakati ya afya kazini kwenye mipango ya kila mwaka ya taasisi, sambamba na kujengeana uwezo wa kukabiliana na changamoto za kiafya katika maeneo ya kazi.

Ameongeza kuwa Tume ya Madini imeendelea kuwa mfano wa kuigwa kwa kuhimiza mazoezi ya viungo kupitia mabonanza, pamoja na kuhakikisha watumishi wenye magonjwa sugu wanapata lishe bora na huduma stahiki.

Akizungumza kuhusu usiri wa taarifa za kiafya, Mhandisi Lwamo amewataka watumishi kuheshimu faragha ya wagonjwa na kuhakikisha taarifa za afya zinatolewa kwa ridhaa ya mhusika pekee, ili kuepuka usambazaji wa taarifa zisizo sahihi.

“Ni muhimu wale walioathirika kutoa taarifa kwa hiari yao ili waweze kusaidiwa ipasavyo. Tunapaswa kuwa na moyo wa huruma na uelewa katika kushughulikia masuala haya,” ameongeza Mhandisi Lwamo.

Kwa upande wake, mmoja wa washiriki wa mafunzo hayo ambaye pia ni Fundi Sanifu wa Migodi kutoka Ofisi ya Afisa Madini Mkazi -Kahama, Jackson Mumanyi, ameishukuru Tume ya Madini kwa kuandaa mafunzo hayo muhimu, akisema yatasaidia kuongeza uelewa na kubadili mitazamo ya watumishi kuhusu kujikinga na magonjwa hayo.

Mafunzo hayo ya siku mbili yanafanyika katika ofisi za Tume ya Madini mkoani Dodoma, yakiwa na lengo la kuandaa waelimisha rika watakaosaidia kusambaza elimu ya afya kazini na kuhimiza tabia za kufanya mazoezi kwa watumishi wote wa Tume.









RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amezindua rasmi Baraza la 11 la Wawakilishi Zanzibar na kutoa mwelekeo wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kipindi cha pili cha Awamu ya Nane, akisisitiza dhamira ya Serikali kuendeleza maendeleo ya kijamii na kiuchumi kwa msingi wa amani, umoja na mshikamano wa kitaifa.

Akizungumza leo tarehe 10 Novemba 2025, katika ukumbi wa Baraza la Wawakilishi Chukwani, Unguja, Rais Dkt. Mwinyi amesema Serikali itaendelea kutekeleza Ilani ya CCM 2025–2030, pamoja na ahadi za kampeni na kuendeleza mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha kwanza cha Awamu ya Nane.

Amesema Serikali itaendeleza mageuzi ya kiuchumi kwa kuimarisha sekta za uzalishaji, uwekezaji, sekta binafsi, na matumizi ya teknolojia za kisasa, ikiwa na lengo la kuongeza ukuaji wa uchumi kutoka asilimia 7 hadi 10 kwa mwaka, kudhibiti mfumko wa bei chini ya asilimia 5, kuzalisha ajira mpya 350,000, na kuongeza kipato cha mwananchi hadi Dola 1,880 kufikia mwaka 2030.

Aidha, Serikali itatekeleza ujenzi wa bandari jumuishi ya Mangapwani, bandari za abiria Mpigaduri, Kizimkazi, Shumba na Wete, pamoja na boti mbili za kisasa za mwendo kasi zitakazohudumia safari kati ya Unguja, Pemba, Tanga na Dar es Salaam.

Katika sekta ya afya, Serikali itajenga hospitali nne za mikoa, kuendeleza ujenzi wa Hospitali ya Saratani Binguni, na kuboresha Hospitali ya Mnazi Mmoja.

Katika elimu, Serikali itajenga madarasa mapya 2,000, shule tatu za sekondari za wasichana kwa kila mkoa, chuo cha kisasa cha ualimu, na kuajiri walimu 7,691.

Rais Dkt. Mwinyi amesema Serikali itaendelea kuimarisha utumishi wa umma kwa kuongeza mafunzo, maslahi na nidhamu ya kazi, huku taasisi za ZAECA na CAG zikiimarisha mifumo ya udhibiti wa rushwa na matumizi sahihi ya fedha za umma.

Ameongeza kuwa Afisi ya Usalama wa Shughuli za Serikali (GSO) itaongoza usimamizi wa nidhamu serikalini.

Vilevile, Serikali itajenga vituo viwili vya utamaduni Unguja na Pemba, kuendeleza michezo, na kukamilisha maandalizi ya AFCON 2027.

Akizungumzia Uchumi wa Buluu, Rais Dkt. Mwinyi amesema Serikali inalenga kuongeza idadi ya watalii wa kimataifa kutoka 800,000 hadi 1,500,000 kwa mwaka, na kwa Kisiwa cha Pemba watalii kuongezeka kutoka 200,000 hadi 300,000 kwa mwaka.

Ameeleza kuwa Serikali itaendeleza uvuvi na kilimo cha mwani kwa kuimarisha miundombinu ya uvuvi, ikiwemo madiko na masoko makubwa ya samaki, pamoja na kuwawezesha wafugaji wa mazao ya baharini kama samaki, matango bahari na kaa kwa njia za kibiashara.

Uzalishaji wa mwani mkavu unatarajiwa kuongezeka kutoka tani 19,715 mwaka 2024 hadi tani 40,000 mwaka 2030.

Serikali pia itaendelea kuwawezesha wananchi kiuchumi kwa kutoa mikopo yenye thamani ya shilingi bilioni 100, na mafunzo ya usimamizi wa fedha za ujasiriamali kwa wazalishaji na wafanyabiashara wadogo.

Aidha, Serikali itaandaa mpango maalum wa vijana wajasiriamali na wabunifu ili kukuza miradi yao na kuzalisha ajira mpya 350,000.

Dkt. Mwinyi amesisitiza kuwa Serikali itaendelea kulinda ustawi wa watu wenye mahitaji maalum, wanawake, watoto na wazee, na kukamilisha ujenzi wa nyumba 4,715 katika maeneo ya Chumbuni, Nyamanzi na Kisakasaka Unguja, pamoja na maeneo mengine ya Pemba.

Katika sekta ya usafiri wa anga, Serikali imelenga kuongeza idadi ya abiria wa ndege kutoka 2,140,986 hadi 2,824,011 kwa mwaka, kujenga vituo viwili vya mafuta ya ndege, karakana ya matengenezo ya ndege, na eneo la maegesho kwa mita za mraba 106,000.

Serikali pia itaendeleza barabara ya kurukia ndege Pemba na kujenga jengo jipya la abiria.

Kwa upande wa sekta ya uzalishaji, Serikali itaanzisha sekta ya taifa ya chakula, kukarabati maghala manne na kujenga vihenge (silos) katika Dunga (Unguja) na Chamanangwe (Pemba) vyenye uwezo wa kuhifadhi tani 60,000 kwa wakati mmoja.

Serikali pia itajenga barabara kuu ikiwemo Tunguu–Makunduchi (km 48), Fumba–Kisauni (km 12), Mkoani–Chake Chake (km 43.5), na barabara za utalii Nungwi (km 12), sambamba na uwekaji wa taa za barabarani katika maeneo mbalimbali ya miji.

Baraza la Wawakilishi Zanzibar linatarajiwa kuanza rasmi shughuli zake tarehe 11 Februari 2026.

Na Mwandishi Wetu
MAWAKILI wa Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Tanzania Bara, John Heche katika shauri la kushikiliwa kwa kiongozi huyo, wameiomba Mahakama iwape siku tatu kwa ajili ya kufanya utafiti na kujipanga kujibu pingamizi za upande wa Jamhuri.

Mawakili hao wakiongozwa na Selemani Matauka akisaidiana na mawakili Fredrick Msacky, Paul Kisabo, Neema Salum, Dorice Kafuku na Maduhu William, waliwasilisha mahakamani ombi kwa niaba ya Heche kuwataka wajibu maombi kumfikisha mahakamani au kumwachilia kwa dhamana.

Wajibu maombi ni Mkuu wa Jeshi la Polisi (Inspector General of Police - IGP), Mkuu wa Upelelezi Kanda Maalumu (Dar es Salaam - ZCO), Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP), Mkuu wa Upelelezi Wilaya ya Kinondoni (RCO), Kamishna Mkuu wa Uhamiaji na Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG).

Kiongozi wa Mawakili hao, Matauka, aliomba siku hizo Novemba 10,2025 mbele ya Jaji Obadia Bwegoge baada ya Wakili wa Serikali Mkuu, Agatha Pima, kuieleza Mahakama kuwa wamewasilisha pingamizi la awali na pia wameshawapatia taarifa ya pingamizi waleta maombi.

"Upande wa wajibu maombi tulipewa nafasi ya kujibu kiapo kinzani, kwa sababu juzi ilikuwa Jumapili, waleta maombi tuliwapa taarifa ya kiapo leo (jana), lakini pia kabla hatujaendelea na kiapo kinzani, tumeleta pingamizi la awali," alidai Wakili Pima.

Baada ya maelezo hayo, Wakili Matauka alidai kuwa ni sahihi kwamba maombi yaliyokuwa mbele yake yaliitwa kwa ajili ya kusikilizwa na kwamba nusu saa iliyopita ndiyo alipewa taarifa hiyo ya kiapo kinzani na wajibu maombi.

"Ni maombi yetu kwa upande wa waleta maombi kwamba kwa sababu kuna pingamizi la awali, tungepewa nafasi ya kufanya utafiti na kujipanga. Naomba iahirishwe kwa ajili ya kwenda kujiandaa kujibu hoja za pingamizi, tunaomba siku tatu ambayo ni Novemba 13, 2025," aliomba Matauka.

Jaji Bwegoge aliuuliza upande wa wajibu maombi kuhusiana na ombi hilo, ambapo Wakili Pima alidai kuwa hawana pingamizi na kwamba wapewe muda wa kujiandaa.

"Waleta maombi wenyewe ndiyo wameomba muda, nahisi wanahitaji muda zaidi wa kujiandaa. Mahakama imeridhia ombi lao, na shauri litaendelea Novemba 13, 2025 saa 4:30 asubuhi," alisema Jaji Bwegoge.

Heche anashikiliwa na polisi tangu Oktoba 22, 2025, alipokamatwa nje ya geti la Mahakama Kuu Dar es Salaam.

Katika taarifa iliyotolewa na Wakili Hekima Mwasipu Novemba 4, 2025, ilieleza kuwa Heche amepewa tuhuma za kujihusisha na vitendo vya kigaidi kutoka Kimara hadi Magomeni na kujihusisha na vitendo vya kigaidi maeneo ya Msewe na External.


MAHAKAMA Kuu Masjala Ndogo Dar es Salaam imeahirisha kesi ya uhaini inayomkabili Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Tundu Lissu hadi Jumatano Novemba 12, 2025 baada ya upande wa Jamuhuri kueleza kuwa Lissu ameshindwa kuletwa kwa sababu za kiuslama.

Mapema leo wakili wa Serikali Mwandamizi, Tawabu Issa akisaidiana na wakili wa serikali Mwandamizi Cathbert Mbilinyi alidai mbele ya jopo la majaji watatu wakiongozwa na Jaji Dunstan Ndunguru akisaidiana na Jaji James Karayemaha na Ferdinand Kiwonde kuwa mshtakiwa Lissu hajaletwa leo na walipofuatilia magereza wameambiwa ni sababu za kiusalama.

"Waheshimiwa majaji, kesi leo ilikuwa inakuja kwa ajili ya kuendelea kusikiizwa, kwa shahidi wa upande wa mashtaka, mshtakiwa Tundu lissu hayupo mahakamani na tumewasiliana na mkuu wa magereza amesema ameshindwa kumfikisha kwa sababu za kiusalama." Amedai Issa.

Amedai kuwa kesi ilikuwa iendelee na uslilizwaji Novemba 3 na kutokana na hali ha kiusalama kutokuwa imetengemamaa huko nje ikapangwa leo (Novemba 10, 2025) kwa ajali ya kuendelea na usikilizwaji....kutokana na hali ya Dar es Salaam kutokuwa kwenye utulivu pia mashahidi waliopaswa kufika kutoka Mbeya na Ruvuma wameshindwa kufika kwa ajili ya maandalizi ya usikilizwaji wa shauri hili.

Amedai kuwa,kufuatia hali hiyo hawakuwa wamepata shahidi kutokana na hali ya usalama wa jiji la Dar es Salaam kutokuwa salama kwa asilimia 100, hivyo akomba shauri hilo liahirishwe kwa siku 14 chini ya kifungu cha sheria cha 302 (1) cha CPA

Kesi hiyo imeahirishwa hadi Novemba 12, 2025 kwa ajili ya kuendelea kusikilizwa. Mahakama imewataka upande wa Jamhuri kuhakikisha siku hiyo wanakuwa na shahidi. Pia imetoa hati ya wito kwa mshtakiwa aletwe mahakamani kwa ajili ya kuendelea na usikilizwaji wa shauri.

MERIDIANBET imeamua kuvunja mipaka kwa kuleta kitu kipya kabisa, Meridianbet Missions. Huu ni mfumo wa kiubunifu unaochanganya michezo ya sloti na ushindani wa kimkakati. Sasa, kila mzunguko unakuwa zaidi ya burudani, ni hatua ya kuelekea mafanikio halisi, zawadi kubwa, na hadhi ya kipekee kwa wachezaji wanaothubutu kufuata misheni yao.

Katika dunia ya Meridianbet Missions, wewe si mchezaji tu, wewe ni mshindani, mpambanaji anayechagua misheni kutoka sloti maarufu kama Gates of Olympus, Ladies Days, Win&Go na nyinginezo. Kila misioni unayokamilisha hukupa pointi maalum zinazokupandisha ngazi kutoka Bronze, Silver, hadi Gold. Kadri unavyopanda juu, ndivyo unavyofungua milango ya zawadi kubwa zaidi, huku kila hatua ikihesabiwa kama ushindi binafsi katika safari yako ya kasino.

Tofauti kubwa ya mfumo huu ni kwamba zawadi zake ni za kweli na za kifahari. Wakati wengine wanazungusha tu sloti kwa matumaini, Meridianbet inakupa sababu ya kucheza zaidi kwa kuwa unaweza kujinyakulia zawadi kama PlayStation 5, Hisense Smart TV, JBL Speaker, iPhone 16, pamoja na mizunguko ya bure na tiketi za kubashiri bure. Hapa, kila juhudi yako inalipwa.

NB; Meridianbet haikuachi nyuma, kuna michezo mbalimbali ya kasino mtandaoni pamoja na mechi za kimataifa za kubashiri zenye odds bomba zinazokuongezea nafasi ya kuongeza kipato chako kila siku. Kujiunga ni rahisi! Tembelea meridianbet.co.tz au piga *149*10#.

Kujiunga na Meridianbet Missions ni kama kufungua mlango wa dunia mpya ya michezo ya sloti. Unachohitaji ni akaunti ya Meridianbet, kisha chagua mchezo unaoupenda, kamilisha misheni, na tazama pointi zako zikikua.

Kwa ulimwengu wa kasino mtandaoni, Meridianbet Mission imekuja na mchanganyiko wa teknolojia, burudani, na ushindi unaoshirikisha kila mchezaji kama shujaa. Jiunge leo, chukua misheni yako, na geuza mizunguko yako kuwa mafanikio na zawadi kubwa.

Na; OWM (KVAU) – Nairobi

Wajasiriamali wa Tanzania wamepongeza Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuwawezesha kushiriki Maonesho ya 25 ya Wajasiriamali Wadogo na wa Kati wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), maarufu kama Nguvu Kazi au Jua Kali, yanayoendelea jijini Nairobi, Kenya.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti, wajasiriamali hao wamesema Serikali imewasaidia kugharamia usafiri pamoja na mizigo yao, jambo ambalo limeongeza ari na hamasa ya kushiriki kwa wingi katika maonesho hayo.

“Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutuwezesha kufika Nairobi. Hii ni fursa ya kipekee kwetu kukuza biashara zetu na kujifunza kutoka kwa wajasiriamali wa nchi nyingine,” amesema mmoja wa washiriki.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Shirikisho la Vyama vya Wajasiriamali Wadogo na wa Kati katika Jumuiya ya Afrika Mashariki upande wa Tanzania (CISO–Tanzania), Josephat Rweyemamu, amesema Serikali imeendelea kuratibu ushiriki wa wajasiriamali hao ili kuwawezesha kutangaza bidhaa na huduma zao nje ya mipaka ya nchi.

Maonesho hayo ya 25 yamebeba kaulimbiu isemayo: “Miaka 25 ya Ujumuishaji wa Jumuiya ya Afrika Mashariki: Kuendeleza Ubunifu na Minyororo ya Thamani ya Kikanda kwa Biashara Ndogo na za Kati Shindani kuelekea Maendeleo Endelevu.”








Na Mwandishi wetu, Amboni-Tanga

Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro inatarajia kuendelea kuimarisha huduma za utalii katika mapango ya Amboni yaliyopo mkoani Tanga ili yaweze kuvutia watalii wengi kutoka maeneo  mbalimbali duniani.

Akizungumza na watumishi wa kituo hicho kaimu Meneja wa Uhusiano kwa umma wa mamlaka hiyo, Afisa Uhifadhi Mkuu Hamis Dambaya amesema kuwa malengo ya kuboreshwa kwa huduma katika mapango ya Amboni yanatokana na mwelekeo mpya wa mamlaka hiyo ya kutaka kuongeza mapato na kutanua wigo wa vivutio vya utalii.

“Ndani ya Mapango tumeweka miundombinu ya taa, njia ya kutembelea wageni, mifumo ya TEHAMA na mazingira ya kupumzika wageni wanaotembelea Mapango haya, barabara ya kuja eneo la Mapango zinapitika vizuri na ujenzi wa geti umekamilika, tutaendelea na jitihada mbalimbali za maboresho ili eneo hili livutie wageni wengi zaidi” alisema Dambaya.

Miongoni mwa huduma zitakazoboreshwa katika eneo hilo ni pamoja na barabara ya kuingia mapango hayo na uanzishwaji  wa mazao mapya ya utalii.

Mapango ya Amboni yaliyopo mkoani Tanga ni moja ya kivutio kikubwa cha utalii kutokana na kuwepo kwa miamba ya asili ambayo inatokana na historia ya kuumbwa kwa dunia. 

Kwa mujibu wa Mkuu wa Hifadhi ya Mapango ya Amboni Afisa Uhifadhi Daraja la Kwanza Ramadhan Rashid, eneo hilo hutembelewa na wastani wa wageni 18,000 kwa mwaka huku idadi hiyo ikitarajiwa kuongezeka kutokana na uboreshaji wa miundombinu ya utalii pamoja na mifumo ya malipo









 

Na. Edmund Salaho -Arusha

Bodi ya Wakurugenzi wa Uendeshaji wa Kampuni Tanzu ya Uwekezaji ya Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA INVESTMENT LTD - TIL) imezinduliwa rasmi leo Novemba 10, 2025 jijini, Arusha na Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini - TANAPA, Mkuu wa Majeshi Mstaafu, Jenerali George Marwa Waitara.

Akizungumza kwa niaba ya Bodi ya Wadhamini ya TANAPA wakati wa uzinduzi wa bodi hiyo Jenerali Waitara aliipongeza bodi hiyo na kuwataka kuimarisha uongozi wa kitaalamu katika usimamizi wa maendeleo ya kampuni hiyo.

"Bodi ya Wadhamini inawapongeza kwa kuchaguliwa kuongoza kampuni hii  twendeni pamoja kusimamia kwa weledi na uwazi miradi yote itakayotekelezwa na Kampuni, tukaimarishe ushirikiano kati ya Kampuni, TANAPA, na wadau mbalimbali kwa misingi ya uwajibikaji, ubunifu na uadilifu."

"Ni matarajio yetu kwamba mtaleta Ubunifu katika uwekezaji unaoleta tija, Ujenzi wa taswira chanya ya Kampuni katika sekta za umma na binafsi, pamoja na Utekelezaji wa miradi inayolingana na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 ikiwemo falsafa ya uhifadhi endelevu na wenye tija kwa Taifa na jamii kwa ujumla" alisema Waitara

Naye, Kamishna wa Uhifadhi TANAPA, CPA. Mussa Nasoro Kuji alibainisha kuwa Shirika linaendelea kutambua mchango mkubwa wa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kuweka mazingira wezeshi ya uwekezaji na mageuzi ya kiuchumi nchini na hususan kwenye eneo la uhifadhi na utalii nchini.

Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya TIL, Mhandisi Dkt. Richard Matolo alibainisha kuwa  Kampuni imejipanga vilivyo katika kuleta mapinduzi katika ukandarasi huku ikijidhatiti kwa utaalamu wa hali juu, pamoja na vifaa vya kutekeleza kazi hizo za ukandarasi.

"TIL tunao wataalamu wenye elimu mbalimbali na uzoefu mkubwa katika kazi hizi za ukandarasi Kampuni inavyo vifaa vingi na vya kisasa. Tunaahidi kuchapa kazi yenye ubora wa hali ya juu". 

TANAPA INVESTMENT LTD (TIL) ni Kampuni Tanzu ya Uwekezaji ya TANAPA ilianzishwa kwa malengo makuu ya Kutekeleza miradi mbalimbali ndani ya Shirika kwa gharama nafuu zaidi na Kutekeleza miradi nje ya Shirika kama kitega uchumi.












Top News