Na Mwandishi Wetu

Kamishna wa Uhifadhi wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Prof. Dos Santos Silayo, amewahimiza Watanzania kutumia kikamilifu fursa zinazopatikana katika sekta ya misitu ili kukuza uchumi, kulinda mazingira na kupambana na mabadiliko ya tabianchi.

Akizungumza jana Julai 7, 2025, katika Maonesho ya 49 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (DITF), Prof. Silayo alisema sekta ya misitu ni kiungo muhimu cha maendeleo kwa kuwa inachangia ukuaji wa sekta nyingine ikiwemo maji, nishati, kilimo na mifugo.

“Misitu ina nafasi ya kipekee katika kupunguza na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi. Kupitia maonesho haya, tunawaeleza wananchi umuhimu wa kuwa na misitu, kuhifadhi na kutumia fursa zilizomo ndani yake kwa maendeleo endelevu,” alisema Prof. Silayo.

Amesema sekta ndogo ya nyuki ni mfano wa jinsi uhifadhi wa misitu unavyoweza kuchochea kipato kwa wananchi kupitia ufugaji nyuki na uzalishaji wa asali, huku ikisaidia kulinda uoto wa asili.

Aidha, Kamishna huyo alisisitiza umuhimu wa uvunaji endelevu wa mazao ya misitu unaochochea ukuaji wa viwanda, hasa vya bidhaa za ujenzi na nishati safi, akibainisha kuwa TFS inaendelea kushirikiana na taasisi nyingine za serikali kutoa elimu ya upandaji miti na uhifadhi wa mazingira.

“Tunaelimisha wananchi kuhusu upandaji wa miti ya kibiashara, miti inayotunza vyanzo vya maji, matunda, dawa na miti kwa ajili ya kivuli mijini ili kukabiliana na hali ya hewa yenye mabadiliko ya mara kwa mara,” alisema Prof. Silayo.

Vilevile, alibainisha kuwa TFS inahamasisha uwekezaji katika utalii ikolojia kwa kutoa fursa kwa wawekezaji kuwekeza kwenye miundombinu ya malazi, michezo ya kitalii kama mbio za nyika, michezo ya magari na pikipiki pamoja na huduma nyingine zinazoweza kuongeza thamani ya misitu.

Prof. Silayo alimshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa mchango mkubwa wa kuutangaza utalii wa Tanzania kupitia filamu za kimkakati zilizowezesha dunia kufahamu vivutio vya nchi na hivyo kuongeza watalii na wawekezaji.

“Tunawaalika Watanzania na wawekezaji wa ndani na nje kufika TFS ili kushirikiana nasi katika kulinda, kuendeleza na kunufaika na sekta ya misitu. Misitu ni urithi wetu na mkombozi wa uchumi na mazingira,” alisisitiza Prof. Silayo.


Daktari Bingwa wa maradhi ya kina mama na Uzazi Ummulkulthum Omar


Na Nihifadhi Abdulla, Zanzibar.
WATAALAMU wa afya wameshauri wazazi kuhakikisha wanawachunguza watoto wao mara tu wanapozaliwa, siyo tu kuangalia afya ya jumla, bali pia sehemu zao za siri, ili kubaini mapema matatizo ya kiafya yanayoweza kuathiri maisha yao baadaye.

Ushauri huu umetolewa kufuatia matukio kadhaa yanayoripotiwa ya baadhi ya watoto kuzaliwa na matatizo kama korodani moja au matatizo ya kuwa na viashiria vya jinsia mbili, hali ambayo kitaalamu hujulikana kama Disorders of Sex Development (DSD).

Daktari Bingwa wa maradhi ya kina mama na Uzazi wa Hospitali ya Mnazimmoja Ummulkulthum Omar amesema mara nyingi wazazi wanapozaliwa mtoto wa kiume hushangilia na kuona kila kitu kipo sawa, lakini hawachunguzi kwa makini hali ya vyumba vya siri vya watoto wao. “Unakuta mtoto amezaliwa ana korodani moja au viashiria vingine vinavyoleta mashaka, lakini watu husema acha akue kwanza. Kumbe tatizo linaweza kuwa kubwa zaidi kuliko wanavyodhani,” amesema Dk. Ummu.

Amefafanua kwamba baadhi ya watoto huzaliwa wakiwa na tatizo la korodani moja, ambalo kitaalamu huitwa undescended testis, ambapo korodani moja inashindwa kushuka kwenye sehemu yake ya kawaida.

Shirika la Afya Duniani (WHO) katika ripoti yao ya Global Health Observatory ya mwaka 2022, ikionyesha kwamba kati ya kila watoto 1,000 wanaozaliwa, angalau 4 hadi 5 wanazaliwa na matatizo ya sehemu za siri vinavyohusiana na jinsia mbili au korodani moja, ingawa kiwango hiki kinaweza kutofautiana kutoka nchi moja hadi nyingine.

Kwa mujibu wa WHO, Disorders of Sex Development (DSD) siyo nadra kama jamii inavyodhani, na takwimu zinaonesha kwamba hali hii hutokea kwa wastani wa mtoto mmoja kati ya kila watoto 4,500 hadi 5,500 wanaozaliwa duniani kote.

Katika ripoti ya Disorders of Sex Development 2023 WHO imesisitiza kwamba “utambuzi wa mapema” ni jambo muhimu kwa sababu matibabu yanapochelewa yanaweza kuleta madhara makubwa kiafya, kisaikolojia na kijamii kwa watoto hawa. “Ni muhimu kila mtoto anayezaliwa kuchunguzwa sehemu zake za siri, siyo kwa sababu tu ya afya ya mwili, bali pia kwa sababu ya ustawi wake wa baadae

Zainab Suleiman, mkaazi wa Jumbi wilaya ya Kati Zanzibar mama wa mtoto aliyezaliwa na korodani moja, ameeleza jinsi alivyopitia changamoto hiyo alijifungua mtoto wa kiume na kufurahia kama wazazi wengine, lakini baadaye aligundua kuna tofauti. “Nilipojifungua niliona mtoto wangu ana korodani moja tu. Wauguzi walisema labda nyingine itashuka baada ya muda. Tulingoja, lakini haikushuka. nilipokwenda tena hospitali madaktari wakanieleza kuwa mtoto ana tatizo ,” amesema Zainab.

Zainab amesema wakati anapata taarifa hizo, moyo wake ulimuuma sana, kwani hakuwahi kufikiria kwamba mtoto wake angekumbwa na hali kama hiyo. “Nilikuwa sijui kabisa haya mambo. nilidhani mtoto wa kiume lazima awe na korodani mbili. Niliona aibu na sikuwa tayari kumwambia mtu,” amesema Zainab

Dk ummulkulthum amesema matatizo kama haya yakigundulika mapema, huwa yana nafasi kubwa ya kutibiwa kwa njia ya upasuaji mdogo au matibabu ya homoni, hivyo kumwepusha mtoto na matatizo makubwa ya kiafya na kisaikolojia anapokuwa mtu mzima.

Amesema iwapo matatizo haya hayataangaliwa mapema, kuna hatari ya kupelekea mtoto kupata saratani kwenye korodani iliyofichika au matatizo ya utambulisho wa jinsia. “Hii siyo hali ya kumcheka mtu. ni jambo la kitabibu linalohitaji huruma, elimu na msaada wa jamii,” amesema Daktari

Baada ya vipimo zaidi, madaktari walimhakikishia Zainab kuwa mtoto wake hana chembechembe za jinsia nyingine na kwamba ni wa kiume, ingawa angehitaji ufuatiliaji wa kitabibu ili kuhakikisha afya yake inaendelea vizuri. “Waliniambia mtoto wangu anaweza kuishi maisha ya kawaida kabisa, lakini lazima awe anakaguliwa mara kwa mara. Namshukuru Mungu na madaktari,” amesema Zainab kwa tabasamu dogo la matumaini.

Kwa upande wake, Zaina Abdalla Mzee, Afisa wa Mradi wa Afya ya Uzazi na Haki za Afya ya Uzazi (SRHR) kutoka TAMWA Zanzibar, amesema taasisi yao imeona kuna haja kubwa ya kutoa elimu kuhusu matatizo ya Afya kwa mama na mtoto kwa vile Zanzibar bado uelewa ni mdogo kuhusu hali hii. “Tunataka jamii ijue kwamba matatizo yeyote kimbilio ni Hospital,” amesema Zaina kwa msisitizo.

Zaina amesema mradi huo unakusudia kutoa elimu katika kliniki za wajawazito na pia kupitia vyombo vya habari ili kufikisha ujumbe kwa watu wengi zaidi. Huku akieleza kuwa wanashirikiana na madaktari ili kutoa elimu sahihi na kuondoa aibu iliyopo kwenye jamii kuhusu matatizo haya. “Tunataka kila mzazi ajue kwamba mtoto anapozaliwa lazima achunguzwe, si kuangalia uso na mikono pekee. Hata sehemu zake za siri lazima ili yapatikane matibabu ya mapema,” amesema Zaina.

Kwa mujibu wa WHO, watoto wenye matatizo kama korodani moja au jinsia mbili wana nafasi kubwa ya kuishi maisha yenye afya bora endapo watapata matibabu mapema na ushauri wa kitaalamu. Shirika hilo limeeleza kuwa kuchelewa kugundua matatizo hayo huongeza uwezekano wa mtoto kupata saratani, matatizo ya uzazi au matatizo ya kisaikolojia yanayoweza kumfanya mtoto ajione hana thamani katika jamii. “Mapema ndiyo tiba,”

Zainab Suleiman anasema changamoto kubwa aliyopitia ilikuwa maneno ya watu na woga wa kutengwa kwenye jamii kuna wakati alikuwa anajilaumu mwenyewe akidhani labda kuna jambo baya alilofanya wakati wa ujauzito. “Nilijilaumu sana. nilidhani labda kuna kitu nilikula au nilikosea. lakini madaktari waliniambia si kosa langu. ni hali ya kimaumbile,” amesema Zainab huku akifuta machozi.

Zainab kwa sasa ana faraja baada ya mtoto wake kuendelea vizuri kiafya na amepata matumaini kuwa ataishi maisha ya kawaida sambamba na kuwaomba wazazi wenzake kutokuwa na aibu kupeleka watoto hospitalini mara wanapoona dalili za hali isiyo ya kawaida. “Mimi nimejifunza. bora aibu kidogo kuliko matatizo makubwa baadaye. wazazi wenzangu tusikae kimya,” amesema Zainab.

Kwa sasa, wataalamu wa afya na taasisi kama TAMWA Zanzibar pamoja na WHO wanaendelea kutoa wito kwa jamii kupeleka watoto hospitalini mara tu wanapozaliwa ili kuhakikisha wanachunguzwa na kugundulika mapema iwapo wana matatizo yoyote. Dk. Ummy amesisitiza kwamba wazazi waache kusema eti mtoto akikua matatizo yatapona yenyewe. “Tuwe na utamaduni wa uchunguzi wa mapema. Hii ni afya ya mtoto wetu na maisha yake ya baadaye,” amemalizia Daktari kwa kutilia mkazo.


Mkurugenzi wa Taasisi ya Miriam Odemba Foundation (MOF) ambaye pia ni mwanamitindo nguli wa kimataifa, Miriam Odemba amesisitiza Watanzania kuchangia fedha kwa ajili ya kufanikisha ujenzi wa vyoo na baadhi ya miundombinu katika Shule ya Misingi Mwendapole iliyopo Kibaha mkoani Pwani.

Hatua hiyo ni juhudi za taasisi hiyo katika kuiunga mkono serikali kuhakikisha wanafunzi wanapata miundombinu bora na imara ya kujisomea.

Odemba amefafanua kauli hiyo, akisema kuwa lengo mojawapo la taasisi yake ni kuhakikisha vyoo vipya zaidi ya 14 vinakamilika, na vingine vitaendelea kukarabatiwa kwa awamu, ikihusisha jumla ya vyoo 36, na miundombinu mingine.

Shule hiyo imekuwa ikiteseka kwa miaka kadhaa sasa kwa changamoto za miundombinu, zinazopelekea binti wa kike kusoma kwenye mazingira magumu.

“Kutuunga kwako mkono ni muhimu, kwani hakuna mchango mdogo wowote unahitajika kufanikisha hili,” amesema Miriam.

Taasisi hiyo imekuwa ikijishughulisha kwa ajili ya kumjengea mazingira wezeshi kwa binti wa kike nchini kusoma na kupanga malengo yake ya baadae, na pia kuchangia maboresho kwenye sekta mbalimbali, ikiwemo urembo, vipaji, sanaa na Elimu.

"Sisi tuna upendo, na tunatamani watanzania wote tuungane kwa pampja katika kuleta mabadiliko chanya kwa ajili ya jamii yetu." alisisitiza Miriam.

Miriam amewaomba watanzania wenye Moyo Jl kuchangia kwa njia ya Simu hata kiasi cha Tshs. 1000 au zaidi kwa namba 0749 808073 jina litatokea MIRIAM ODEMBA FOUNDATION au kwa Benki ya NBC Acount Namba 011172000038

*Aweka mikakati ya kuinua vijana katika mafunzo ya ufundi stadi

Na Mwandishi Wetu 
Mamlaka ya Elimu Mafunzo ya Ufundi (VETA) imesema kuwa kuna mageuzi katika utoaji wa mafunzo ya ufundi yanayochochea katika kuandaa nguvu kazi katika viwanda pamoja kuongeza fursa za ajira kwa vijana za kujiajiri au kuajiriwa.

Hayo ameyasema Mkurugenzi Mkuu wa VETA CPA Anthony Kasore wakati alipotembelea Banda la VETA kwenye maonesho ya Biashara Kimataifa yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere (Sabasaba) jijini Dar es Salaam.

CPA Kasore amesema kuwa katika mageuzi ya VETA ni kuleta fani zinazoendana na mahitaji yaliyopo katika mazingira yanayozunguka jamii katika kutatua changamoto zinazotokana na kukosekana kwa mafunzo ya ujuzi na ufundi Stadi.

Aidha amesema katika ufundishaji wa wanafunzi ni tofauti kwani anaanza kulijua soko akiwa katika mafunzo na anapohitimu anaingia moja kwa moja katika ajira au kujiajiri.

Amesema kuwa kuna wahitimu wa vyuo ambao wamepata ujuzi ambao wameanza kuzalisha bidhaa na kuingiza katika soko kwa kupata wanunuzi.

Aidha amesema kuwa wajasiriamali wanaongia kwenye mafunzo ya kutengeneza bidhaa mbalimbali wanaongeza thamani ya bidhaa hizo na kupata tija ya kuongeza kipato.

CPA Kasore amesema Serikali ya Awamu ya Sita Chini ya Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan vyuo 80 vimejengwa na vyuo 65 viko katika hatua za ujenzi awali ambapo vyuo hivyo vitakuwa 145 nchi nzima.

Amesema kuwa katika Sekta ya kilimo wamekuja na bunifu ya mashine ya kupukuchulia mahindi na sekta mifugo wamekuja na mashine ya kutengeneza vyakula vya kuku pamoja na mashine ya kutotoleshea vifaranga.

Hata hivyo amesema VETA imeanzisha kampuni Tanzu ambapo bunifu hizo zitapatikana kwa kuuzwa lengo ikiwa ni kuendeleza bunifu hizo kwa kufanya kazi na sio kuzifungia.

Amesema tofauti ya maonesho hayo VETA imekuja na vitu ambavyo wanaweza kujifunza watoto katika kuwaandaa mapema katika ujuzi.

Amesema Sera ya Elimu iliyozinduliwa inatoa majibu ya namna ya kufanya mafunzo ya ufundi Stadi yanakwenda kuchochea uchumi kwa vijana wa kitanzania.








 Mkurugenzi wa VETA CPA Anthony Kasore akiwa katika picha mbalimbali za kutembeleea Banda la VETA ,Sabasaba jijini Dar es Salaam.
SHIRIKA la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) limeibuka mshindi katika Maonesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam, maarufu kama Sabasaba, baada ya kutuzwa kwa mchango wake mkubwa katika kulinda mazingira kupitia matumizi ya nishati safi.

Akizungumza mara baada ya kupokea tuzo hiyo, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano wa TPDC, Bi. Maria Mselemu, alisema mafanikio hayo ni matokeo ya utendaji kazi wa hali ya juu na ufuatiliaji makini wa shughuli za shirika hilo.

"Hii ni tuzo yetu ya tano katika maonesho haya, na kwetu sisi imekuwa kawaida kupata tuzo kutokana na ubora wa huduma na miradi yetu, ikiwemo tuzo ya mazingira tuliyopokea leo," alisema Bi. Mselemu.

Alifafanua kuwa TPDC imefanikiwa kupunguza kwa kiasi kikubwa utoaji wa hewa ukaa kwa kutumia nishati safi ya kupikia na ile inayotumika katika magari, hatua ambayo imechochea mafanikio yao katika nyanja za mazingira.

"Kupitia matumizi ya nishati safi, tumeweza kuondoa zaidi ya tani 100,000 za hewa ukaa. Hii ni hatua kubwa katika kulinda mazingira yetu. Tunajivunia kuwa sehemu ya suluhisho la mabadiliko ya tabianchi," aliongeza Bi. Mselemu.

Maonesho ya Sabasaba yanayofanyika kila mwaka katika Viwanja vya Mwalimu Nyerere, Dar es Salaam, yanawakutanisha washiriki kutoka sekta mbalimbali za biashara na maendeleo, yakilenga kuonyesha bidhaa na huduma bora kutoka Tanzania na mataifa mbalimbali duniani.








Na Mwandishi Wetu

SHULE ya Sekondari St Anne Marie Academy imekuwa miongoni mwa shule zilizofanya vizuri zaidi kwa mara nyingine tena kwenye matokeo ya kidato cha sita mwaka huu kwa kufaulisha wanafunzi wengi kwa daraja la kwanza na la pili.

Kwenye matokeo hayo yaliyotangazwa na Baraza la Taifa la Mitihani NECTA jana, wanafunzi 51 wa shule hiyo iliyoko Mbezi Kimara kwa Msuguli walipata daraja la kwanza, wanafunzi 84 daraja la pili na wanafunzi 74 daraja la tatu.

Mkuu wa shule hiyo Edrick Phillemon alielezea kufurahishwa na matokeo hayo akisema kuwa shule hiyo imekuwa ikipokea wanafunzi wenye wastani wa kawaida na kuhakikisha wanawafundisha hadi kupata daraja la kwanza na la pili na wachache sana daraja la tatu.

Alisema tofauti na shule zingine zinazochukua wanafunzi wenye ufaulu mkubwa, St Anne Marie imekuwa ikichukua wanafunzi wa kawaida bila kubagua hata wenye wastani mdogo kwa kuwa inajiamini kuwa na walimu mahiri wenye uwezo wa kuwaandaa kwaajili ya mitihani ya mwisho na wakafanya vizuri.

“Kwetu haya ni matokeo mazuri sana ukizingatia sisi hatubagui wanafunzi tunachukua wenye wastani wa kawaida sana kwasababu tunawaamini walimu wetu ambao wanafanyakazi usiku na mchana, mwanafunzi akija kwetu hata awe na wastani mdogo kwenye mtihani wake wa mwisho atafanya vizuri kwasababu ya umahiri wa walimu wetu na miundombinu mizuri ya shule,” alisema

“Kipekee nampongeza Mkurugenzi wa shule ya St Anne Marie Academy Dk Jasson Rweikiza kwa kuiwezesha shule hii kuwa na miundombinu ya kisasa kama maktaba zenye viyoyozi, maabara, madarasa na walimu mahiri wa masomo yote na haya kwa ujumla ndiyo siri ya mafanikio ya shule hizi,’ alisema

“Hata lishe ya wanafunzi hapa St Anne Marie Academy ni ya kipekee wanafunzi wanakula hadi milo minne kwa siku tuna bustani za mboga mboga matunda, Mkurugenzi ameweka utaratibu wa motisha kwa walimu na wanafunzi wanaofanya vizuri kwenda kwenye mbuga za wanyama kama Setengeti, Ngorongoro na Mikumi na kupewa fedha taslim motisha kama hii ni miongoni kwa vichocheo vya sisi kupata matokeo mazuri,” alisema

Alisema Mkurugenzi wa shule hiyo amekuwa msaada mkubwa kwa kuweka bodi ya mitihani shuleni hapo ambayo kazi yake ni kutunga mitihani na kufuatilia maendeleo ya taaluma ya wanafunzi wa shule hiyo.

Hivi karibuni Mkurugenzi na Mwanzilishi wa shule hiyo, Dk Jasson Rweikiza, alisema shule hiyo iliamua kuweka bodi ya mitihani shuleni hapo ili kuongeza ubora wa taaluma.

“Mwalimu hapa St Anne kazi yake ni kufundisha kazi ya kutunga mitihani imepewa bodi ya mitihani kwasababu tuliona mwalimu akifunsisha mwenyewe akatunga mitihani mwenyewe anaweza kupendelea kwenye silabasi alizofundisha tu akaacha zile ambazo hakuzikamilisha,” alisema

“Sasa bodi ikitunga mitihani kama silabasi zilikuwa tano watatunga mtihani kwenye silabasi zote na mwanafunzi akifeli mwalimu atapaswa kujieleza kwanini wanafunzi wamefeli mtihani wake,” alisema Dk. Rweikiza


-Mkurugenzi Mkuu REA abainisha hatua zinazochukuliwa

-Amshukuru Rais Samia kwa kuwezesha

Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Hassan Saidy amesema Wakala umejizatiti kuhakikisha 80% ya Watanzania wanatumia Nishati Safi ya Kupikia ifikapo mwaka 2034 kama ilivyoelekezwa katika Mkakati wa Taifa wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia.

Amebainisha hayo Julai 07, 2025 katika Maonesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa (Sabasaba) Jijini Dar es Salaam ndani ya Banda la Maonesho la Wakala wa Nishati Vijijini (REA).

“REA inalo jukumu la kuhakikisha maeneo yote ya vijijini yanapata aina zote za nishati safi zinazotumika nchini ikiwemo; umeme, nishati safi ya kupikia pamoja na bidhaa za mafuta ya petroli na dizeli na hili linafanyika kupitia miradi mbalimbali ambayo baadhi imekamilika na mingine ipo katika hatua tofauti tofauti za utekelezaji,” amebainisha Mha. Saidy.

Alisema Mkakati wa Taifa wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia umeelekeza ifikapo mwaka 2034; angalau 80% ya Watanzania wawe wanatumia nishati safi ya kupikia na REA ni miongoni mwa taasisi zilizopewa jukumu la kuhakikisha lengo hilo linafikiwa.

Alibainisha kuwa kwa sasa takriban asilimia 96 ya wananchi maeneo ya vijijini wanatumia kuni na mkaa kupikia na kwamba jukumu lililopo ni kuhakikisha wananchi hao wanaachana na matumizi ya nishati zisizo salama na kuanza kutumia nishati safi na salama.

Alitaja hatua mbalimbali zinazoendelea kuchukuliwa na REA ikiwemo uhamasishaji na uelimishaji wananchi kufahamu athari za kutumia nishati isio salama pamoja na kuwafahamisha faida za kutumia nishati safi ya kupikia, kuwarahisishia wananchi upatikanaji wa bidhaa za nishati safi jirani na maeneo yao na kuwezesha teknolojia za nishati yenyewe.

“Kuna dhana imejengeka kwamba nishati safi ya kupikia ni gharama kuliko nishati zingine dhana ambayo haina ukweli kwa 100% kwani kwa sasa kuna teknolojia zilizoboreshwa ambazo zinazuia upotevu wa nishati wakati wa kupika hivyo kuwapunguzia gharama watumiaji," alifafanua Mha. Saidy

Aliongeza kuwa watu wengi hawaangalii gharama nyingine kama muda wanaotumia kusaka kuni na madhila mengine wanayokutana nayo huko porini wakati wakisaka kuni.

Alimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuiwezesha REA kutekeleza jukumu la kusimamia upatikanaji wa nishati safi ya kupikia hasa ikizingitiwa kuwa yeye ni kinara wa nishati safi ya kupikia.

Alibainisha baadhi ya mafanikio ambayo yamepatikana tangu kuanza kutekeleza mkakati huo wa Taifa wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia ambayo ni pamoja na kuwezesha wananchi maeneo mbalimbali vijijini kuhama kupitia ruzuku iliyotolewa ya asilimia 50 kwenye majiko ya gesi ya kilo 6 na vichomeo vyake.

“Serikali inayoongozwa na Mhe. Rais Samia ilitoa ruzuku ya 50% kwenye mitungi ya gesi ya kupikia ipatayo 452,000 ambayo imeshaanza kusambazwa kwenye mikoa yote Tanzania Bara na zoezi linaendelea; sambamba na mitungi 110,000 ambayo ilisambazwa mwaka juzi kupitia Wabunge kwenye majimbo yao,” alisema Mhandisi Saidy.

Sambamba na hilo, Mha. Saidy alibainisha kuwa REA imewezesha Jeshi la Magereza ambapo kwa sasa magereza zote 129 zimehama kutoka kwenye matumizi ya nishati zisizo salama, na hivi karibuni REA imekuja na mpango wa kuwezesha Maafisa wa Jeshi la Magereza nao kutumia nishati safi ya kupikia katika familia zao.

“Kama mtakumbuka Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan alielekeza taasisi zinazohudumia zaidi ya watu 100 zianze kutumia nishati safi ya kupikia na hili tunatekeleza na tunatarajia kuzifikia zaidi ya taasisi 400 katika mwaka huu wa fedha. Tulianza na Jeshi la Magereza, Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) na takriban shule 53,” alibainisha Mha. Saidy.

Mhandisi Saidy vilevile alibainisha mradi wa mikopo nafuu wa kuwezesha ujenzi na uendeshaji wa vituo vya mafuta ya petroli na dizeli ulioanzishwa na REA ambao umelenga kuwasogezea wananchi wa vijijini huduma kwa gharama nafuu na ubora unaokubalika.




RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi,Dkt.Hussein Ali Mwinyi, amesema kuwa katika kipindi hiki cha mabadiliko, Serikali inaendelea kufanya marekebisho ya sera kwa lengo la kuimarisha mazingira ya uwekezaji na kukuza uchumi wa Taifa.

Miongoni mwa hatua zinazochukuliwa na serikali ni kuhakikisha sera mpya zinatoa msukumo wa kuitambulisha Tanzania kupitia bidhaa na huduma zake, na hivyo kuongeza mapato ya Taifa.

Mwinyi alitoa agizo hilo jana katika ufunguzi wa Maonesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa yanayofanyika katika viwanja vya Mwalimu Nyerere jijini Dar es Salaam alisema wizara zinatakiwa kuhakikisha kuwa elimu ya alama za utambulisho wa bidhaa (branding) inawafikia Watanzania wengi, ikiwa ni chachu ya kuongeza thamani ya bidhaa za ndani na kuhamasisha uzalendo wa kiuchumi.

Alisema ni vema wananchi wapende kutumia bidhaa za ndani, kwani ni njia bora ya kukuza uchumi wa kitaifa na kujenga kujivunia bidhaa zetu wenyewe.

"Hatua za kimkakati zinazotekelezwa zinaenda sambamba na kukuza ubunifu, kushirikiana na sekta binafsi, na kuanzisha madirisha ya kupokea maoni kutoka kwa wadau mbalimbali, yote haya yakiwa ni katika kujenga mazingira wezeshi ya biashara na uwekezaji,"alisema

Rais Dkt.Mwinyi alitoa pongezi kwa kuandaliwa kwa mpango kabambe wa uendelezaji wa biashara na kubainisha kuwa uwanja wa kisasa wa biashara unaotarajiwa kujengwa utazingatia mfumo wa ubia kati ya sekta ya umma na sekta binafsi (PPP),na jitihada zikifanywa kuondoa urasimu unaokwamisha maendeleo.

Kw upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Biashara Tanzania (TanTrade), Latifa Khamis, alisema Maonesho ya 49 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (DITF) mwaka huu yameendeshwa kwa njia ya kidijitali kutokana na mifumo ya kisasa iliyowekwa.




Latifa alisema hatua hiyo ni sehemu ya mabadiliko kuelekea maonesho ya miaka 50 (Golden Jubilee) mwaka ujao, ambapo TanTrade imejipanga kuyafanya kuwa ya kisasa zaidi na yenye viwango vya kimataifa.




Latifa alisema kuwa pamoja na uendeshaji wa kidijitali, mipango iliyopo sasa ni pamoja na uboreshaji wa miundombinu ya eneo la maonesho ili kulifanya kuwa la kuvutia zaidi kwa washiriki wa ndani na nje ya nchi.




Naye Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, alisema mkoa wake unayachukulia Maonesho ya Kila Mwaka ya Kimataifa ya Dar es Salaam kama kielelezo cha mkoa huo kimataifa, na hivyo wataendelea kuyaenzi na kuyaboresha.

Alisema Serikali ya mkoa wake itaendelea kushirikiana na Mamlaka ya Kuendeleza Biashara Tanzania (TanTrade) kuboresha miundombinu ya viwanja vya Sabasaba ili iendane na hadhi ya maonesho hayo.

Chalamila alisema wamepanga kuhakikisha kuwa wafanyabiashara wanaokuja kwenye maonesho hayo wanafurahia mandhari ya maeneo ya maonesho, ili waendelee kushiriki kwa muda mrefu.




Naibu Waziri wa Madini Dkt. Steven Kiruswa akizungumza kwenye mkutano na waandishi wa habari Julai 7,2025 katika Mgodi wa Barrick Bulyanhulu - Picha : Kadama Malunde

Rais na Ofisa Mtendaji Mkuu wa Barrick, Mark Bristow akizungumza kwenye mkutano na waandishi wa habari Julai 7,2025 katika Mgodi wa Barrick Bulyanhulu.


*
Serikali imepongeza uwekezaji mkubwa uliofanywa na Kampuni ya Barrick inayoendesha shughuli zake nchini kwa ubia na Serikali kupitia kampuni ya Twiga katika kipindi cha miaka mitano kwa kuwa unachagia kwa kiasi kikubwa katika pato la Taifa na kunufaisha wananchi.


Akiongea na waandishi wa habari mgodini Bulyanhulu, Julai 7,2025 Naibu Waziri wa Madini Dkt. Steven Kiruswa, amesema ubia huu ni wa mfano wa kuigwa katika uwekezaji nchini kwa kuwa mafanikio yake ni makubwa na migodi ya Twiga na Barrick inaendeshwa kwa weledi mkubwa na kutumia teknolojia za kisasa zenye kuleta tija na ufanisi na kuchangia ukuaji wa uchumi wa kijamii nchini kwa ujumla.

Naibu Waziri wa Madini Dkt. Steven Kiruswa


Kwa upande wake, Rais na Ofisa Mtendaji Mkuu wa Barrick, Mark Bristow, amesema ubia huo umejenga mfano endelevu wa uendelezaji wa rasilimali madini nchini tangu uanzishwe na na kuipa sura mpya nafasi ya sekta ya madini katika maendeleo ya taifa, ukizidi kuongeza thamani ya pamoja, ubora wa kiuendeshaji na uwekezaji wa muda mrefu kwa mustakabali wa nchi.


“Tulipoanzisha Twiga, lengo lilikuwa zaidi ya kusuluhisha changamoto za kihistoria. Lilikuwa kujenga mustakabali mpya kwa kuufungua utajiri wa dhahabu wa Tanzania kwa njia inayogawanya kwa haki manufaa yake na kujenga thamani ya kudumu kwa wadau wote. Baada ya miaka mitano, tumeirejesha Barrick katika hali ya kuwa mchangiaji mkubwa katika uchumi wa nchi kwenye sekta hii, huku tukitambuliwa kitaifa katika nyanja mbalimbali kuanzia usalama, matumizi ya bidhaa na huduma za ndani, hadi elimu na miundombinu,” amesema Bristow.





Tangu Barrick ichukue rasmi jukumu la uendeshaji wa migodi mbalimbali nchini mnamo mwaka 2019, kampuni hiyo imeingiza dola bilioni 4.79 katika uchumi wa Tanzania, ikiwa ni pamoja na dola milioni 558 katika nusu ya kwanza ya mwaka 2025 pekee. Zaidi ya asilimia 90 ya ununuzi wa bidhaa na huduma umeendelea kufanyika kutoka kampuni za Kitanzania, ambapo nyingi kati ya hizo ni za wazawa, huku asilimia 95 ya wafanyakazi wake wakiwa Watanzania na asilimia 49 wakitoka katika jamii zinazozunguka migodi.


Rais na Ofisa Mtendaji Mkuu wa Barrick, Mark Bristow.


Mfano wa kuigwa wa hatua zinazochukuliwa na ubia wa Twiga ni Mpango wa Kusongesha Mbele Mustakabali wa Elimu, ambao ni uwekezaji wa pamoja wa dola milioni 30 kati ya Barrick na Serikali ya Tanzania kupitia Ofisi ya Rais, unaolenga kupanua miundombinu ya shule nchini. Mpango huu, sasa ukiwa katika awamu ya pili, unatarajiwa kuwapatia vyumba vya madarasa wanafunzi zaidi ya 45,000.


Migodi ya Barrick nchini Tanzania imeendelea kutoa uzalishaji kulingana na makadirio. Katika mgodi wa Bulyanhulu, utengenezaji wa njia ya chini kwa chini katika eneo la Magharibi Juu umepiga hatua kubwa ya maendeleo yakiimarishwa na ujio wa mitambo mipya na upanuzi wa miundombinu. Uwekezaji maalumu kwenye mifumo ya uingizaji hewa na upunguzaji maji umeboresha ufanisi, kuondoa vikwazo na kuuwezesha mgodi kuzalisha dhahabu zaidi kwa miongo ijayo.


Katika mgodi wa North Mara, mfumo mpya wa kuhifadhi umeme kwa betri uliozinduliwa hivi karibuni umesaidia kuboresha upatikanaji wa nishati, huku shughuli za uchimbaji chini ya ardhi na kwenye machimbo ya wazi zikiendelea kama zilivyopangwa. Shughuli za kuwahamisha watu makazi zimekaribia kukamilika, na Barrick inaendelea kujenga imani na kukubalika kwa uendeshaji wa shughuli zake katika jamii.


“Ushirikiano wetu na jamii zinazotuzunguka ni msingi wa kuwepo kwetu nchini Tanzania. Tumelazimika kufanya kazi kwa bidii ili kuurejesha uhusiano huo, hususan katika eneo la North Mara, na sasa tunaona matokeo chanya ya mawasiliano endelevu na utekelezaji wa ahadi zetu,” amesema Bristow.


Wakati huohuo, Barrick inaendelea kuwekeza kikamilifu katika utafutaji wa madini katika maeneo mapya ya uchimbaji ili kuhakikisha uendelevu wa mustakabali wa shughuli zake nchini. Programu za uchorongaji zinaendelea kulenga kuongeza hifadhi ya madini katika maeneo ya Gokona na Gena ndani ya mgodi wa North Mara, na katika miamba ya Tabaka la aina ya 1 na Tabaka la aina ya 2 katika eneo la Bulyanhulu. Pia, ufuatiliaji na uchorongaji wa kijiofizikia kwa kutumia njia ya upepo umepangwa kufanyika katika maeneo mapya ya Siga na Nzega.


Hata katika mgodi wa Buzwagi, ambao sasa uko katika hatua ya kufungwa, jitihada zinaendelea kuelekezwa katika kuleta thamani ya muda mrefu. Ukanda Maalumu wa Kiuchumi unaandaliwa katika eneo hilo, huku wawekezaji kadhaa wakiwa tayari wameonesha nia. Chuo cha Barrick kinatarajiwa kutoa mafunzo kwa wasimamizi na mafomeni zaidi ya 2,800 kutoka maeneo mbalimbali ifikapo mwishoni mwa mwaka huu, hivyo kuendeleza mchango wa Barrick katika kukuza vipaji vya sekta ya madini barani Afrika.


“Dhamira yetu kwa Tanzania haikukoma pale mawe ya dhahabu yalipoisha kule Buzwagi. Tunaacha tumeweka miundombinu na taasisi zitakazonufaisha taifa kwa muda mrefu ujao,” amesema Bristow.


Akihitimisha maelezo yake kuhusu safari ya miaka mitano ya Twiga, Bristow amesema ubia huo haukusaidia tu kurejesha utulivu wa uendeshaji wa migodi bali pia umejenga msingi wa ustawishaji wa thamani ya muda mrefu kupitia umiliki wa pamoja, uwezeshaji wa wenyeji, na mkabala wa kiuwajibikaji wa kuleta maendeleo.


“Twiga ni zaidi ya kampuni; ni mfano wa kile ambacho sekta ya madini inaweza kuwa pale shughuli zinapotekelezwa kwa usahihi, kwa ubia na kwa malengo,” amehitimisha.

Naibu Waziri wa Madini Dkt. Steven Kiruswa akizungumza kwenye mkutano na waandishi wa habari Julai 7,2025 katika Mgodi wa Barrick Bulyanhulu

Naibu Waziri wa Madini Dkt. Steven Kiruswa akizungumza kwenye mkutano na waandishi wa habari Julai 7,2025 katika Mgodi wa Barrick Bulyanhulu

Naibu Waziri wa Madini Dkt. Steven Kiruswa akizungumza kwenye mkutano na waandishi wa habari Julai 7,2025 katika Mgodi wa Barrick Bulyanhulu

Rais na Ofisa Mtendaji Mkuu wa Barrick, Mark Bristow akizungumza kwenye mkutano na waandishi wa habari Julai 7,2025 katika Mgodi wa Barrick Bulyanhulu.

Rais na Ofisa Mtendaji Mkuu wa Barrick, Mark Bristow akizungumza kwenye mkutano na waandishi wa habari Julai 7,2025 katika Mgodi wa Barrick Bulyanhulu.

Rais na Ofisa Mtendaji Mkuu wa Barrick, Mark Bristow akizungumza kwenye mkutano na waandishi wa habari Julai 7,2025 katika Mgodi wa Barrick Bulyanhulu.

Rais na Ofisa Mtendaji Mkuu wa Barrick, Mark Bristow akizungumza kwenye mkutano na waandishi wa habari Julai 7,2025 katika Mgodi wa Barrick Bulyanhulu

Rais na Ofisa Mtendaji Mkuu wa Barrick, Mark Bristow akizungumza kwenye mkutano na waandishi wa habari Julai 7,2025 katika Mgodi wa Barrick Bulyanhulu.

Meneja wa Barrick nchini Dkt. Melkiory Ngido akizungumza kwenye mkutano na waandishi wa habari Julai 7,2025 katika Mgodi wa Barrick Bulyanhulu.

Mkuu wa wilaya ya Kahama Frank Mkinda akizungumza kwenye mkutano na waandishi wa habari Julai 7,2025 katika Mgodi wa Barrick Bulyanhulu.



Top News