Na Mwandishi Wetu.

Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Queen Sendiga, amezindua rasmi vifaa maalum (KIT) vitakavyotumiwa na washiriki wa Manyara Tanzanite Marathon 2026, huku idadi ya watu waliojiandikisha kushiriki mbio hizo za hisani ikifikia 2,200.

Uzinduzi wa KIT hiyo, inayojumuisha T-shirt, kofia na namba za washiriki, umefanyika Agosti 17, 2026, mjini Babati, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya mwisho kuelekea mbio hizo zinazotarajiwa kufanyika Agosti 22, 2026.

Manyara Tanzanite Marathon 2026 imeandaliwa ikiwa na lengo la kuchangisha fedha zitakazosaidia kuboresha huduma za afya kwa watoto njiti katika Mkoa wa Manyara, hususan katika maeneo yanayohitaji miundombinu na huduma bora zaidi kwa watoto wanaozaliwa kabla ya muda.

Kaulimbiu ya mbio hizo mwaka huu ni “Hatua Moja, Okoa Maisha ya Mtoto,” inayolenga kuhamasisha wananchi, taasisi, kampuni na wadau mbalimbali kushiriki katika tukio hilo huku wakitoa mchango wa moja kwa moja katika kuboresha maisha ya watoto njiti.

Akizungumza katika uzinduzi huo, RC Sendiga amehimiza wananchi na wadau mbalimbali kuendelea kujitokeza kwa wingi kushiriki mbio hizo, akieleza kuwa mwitikio wa watu 2,200 waliojisajili hadi sasa ni ishara ya namna jamii inavyoguswa na ajenda ya kuboresha afya na ustawi wa watoto.

Idadi hiyo ya washiriki inatarajiwa kuongezeka kadri siku ya mbio inavyokaribia, huku waandaaji wakiendelea kutoa wito kwa watu ambao bado hawajajisajili kutumia fursa hiyo kushiriki katika tukio lenye lengo la kuchangia ustawi wa watoto na maendeleo ya afya mkoani Manyara.

Mbali na kushiriki katika mbio hizo, tukio hilo limeandaliwa pia kwa namna inayolenga kukuza utalii wa ndani na kuifanya Manyara kuwa sehemu ya kuvutia kwa wageni kutoka ndani na nje ya Tanzania. Washiriki watakaokuwa wamechagua kifurushi kinachojumuisha ziara ya utalii watapata fursa ya kutembelea Hifadhi ya Taifa ya Tarangire baada ya kumalizika kwa mbio.

Uhusiano kati ya mbio hizo na utalii unalenga kuwapa washiriki uzoefu mpana zaidi, huku ukiendelea kutangaza vivutio vya utalii vilivyopo mkoani Manyara na kuchochea shughuli za kiuchumi zinazotokana na utalii.

Manyara Tanzanite Marathon imeendelea kujijenga kama moja ya matukio yanayounganisha michezo, afya, utalii na uwajibikaji kwa jamii. Kupitia mbio hizo, waandaaji wanatarajia kuhamasisha watu kutoka makundi mbalimbali kushiriki katika jitihada za kuchangia huduma za afya kwa watoto njiti.

Kwa mwaka 2026, msisitizo umewekwa katika kaulimbiu “Hatua Moja, Okoa Maisha ya Mtoto,” huku fedha zitakazopatikana kupitia mbio hizo zikilenga kusaidia ujenzi na uboreshaji wa huduma kwa watoto njiti katika Mkoa wa Manyara.

Uzinduzi wa KIT hiyo umeongeza hamasa kuelekea Agosti 22, ambapo Babati inatarajiwa kuwa kitovu cha tukio hilo litakalowakutanisha washiriki, wadau wa afya, taasisi, wafanyabiashara, watalii na wananchi kwa ujumla katika hatua ya pamoja ya kuokoa maisha ya watoto njiti.


WADAU wa Forodha wakiwemo Mawakala wa Forodha na Maafisa Forodha Mkoa wa Kigoma wamejengewa uwezo kuhusiana na mabadiliko yaliyofanywa na Serikali kupitia Sheria ya Fedha ya mwaka 2026 pamoja na taratibu Forodha.

Elimu hiyo imelenga kuwawezesha
Wadau wa Forodha kuwa na uelewa wa pamoja juu ya Sheria, kanuni na taratibu za forodha na kuwawezesha kutimiza majukumu yao kwa ufanisi na kulipa kodi za Serikali kwa usahihi ili kurahisisha ufanyaji wa biashara na kukuza uchumi nchini.

Elimu hiyo imetolewa na Allan Maduhu, Afisa Forodha Mkuu na Hassan Minga, Afisa Mfawidhi Forodha-Dodoma ambao wamewataka wadau wa Forodha kufuata sheria na taratibu ili kuwawezesha kutekeleza sheria mpya ya Fedha ya mwaka 2026 ikiwemo kufahamu misamaha mbalimbali iliyotolewa na serikali kwa lengo la kuchochea sekta za uzalishaji pamoja na ukuaji wa viwanda nchini.

Misamaha iliyotolewa ni pamoja na msamaha wa Kodi ya Ongezeko la Thamani kwenye nyuzi za kutengenezea nyavu za uvuvi, nyavu za uvuvi zilizozalishwa na wazalishaji wa nyavu za uvuvi nchini pamoja na vifungashio vya maziwa kwa ajili ya kuchochea sekta ya maziwa nchini.

Aidha, Kaimu Meneja Msaidizi wa Forodha Mkoa wa Kigoma Mohamed Mnonda, amesema kulingana na shughuli za Forodha wamejipanga kutekeleza Sheria ya Fedha 2026 ili kuongeza uwajibikaji na ufanisi wa kiutendaji ili kuwezesha na kuboresha ufanyaji wa Biashara mkoani Kigoma.

Kwa upande wa Mawakala wa Forodha wakiongozwa na Dunia Salutwe, wameahidi kufuata sheria na taratibu za Forodha na kuhakikisha wateja wao ambao ni waagizaji na wasafirishaji nje wa bidhaa wanalipa kodi stahiki.


Na Mwandishi Wetu


SERIKALI imedhamiria kuendelea kuimarisha afua za masuala ya UKIMWI nchini kwa kuboresha mazingira ya utekelezaji wa shughuli hizo, huku ikihimiza ushirikiano na wadau mbalimbali katika kuendeleza mapambano dhidi ya UKIMWI.

Kauli hiyo imetolewa na Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Dkt. Jim Yonazi, alipotembelea na kujionea utekelezaji wa shughuli zinazotekelezwa na vikundi vya watu wanaoishi na Maambukuzi ya Virusi vya UKIMWI katika Wilaya ya Nyamagana, Jijini Mwanza.

Akiwa katika ziara hiyo, Dkt. Yonazi amesema Serikali imeendelea kuboresha mazingira na kutenga bajeti inayosaidia kuratibu na kutekeleza afua za masuala ya UKIMWI nchini, huku ikishirikiana na wadau mbalimbali

“Ushirikiano ni muhimu sana kwani, tunaamini unauwezo wa kutuvusha katika mapambano dhidi ya VVU, ambapo tumeendelea kuunganisha nguvu pamoja katika mapambano hayo,” alisema Dkt. Yonazi.

Aliongeza kuwa Ofisi ya Waziri Mkuu, yenye dhamana ya kuratibu shughuli zote za Serikali, ikiwemo masuala ya UKIMWI, itaendelea kuhakikisha vifaa na huduma zinatolewa kwa wakati na ubora kwa WAVIU, huku kanuni na taratibu za afya zikizingatiwa.

Dkt. Yonazi Ametumia jukwaa hilo kuiasa jamii kuendelea kupima afya ili kujitambua na kuchukua hatua za mapema endapo mtu atabainika kuwa na maambukizi ya VVU, ili aweze kuishi kwa tahadhari na kuwalinda wengine.

Kwa upande wake Katibu Tawala Mkoa wa Mwanza, Ndugu Balandya Elikana, amesema kuwa mkoa umechukuwa hatua madhubuti kuimarisha mapambano dhidi ya UKIMWI kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa sekta ya afya na kamati za utekelezaji wa mikakati ya kuzuia maambukizi, huku wakihimiza upatikanaji wa huduma bora na elimu kwa jamii.

“Jamii inaendelea kuhamasishwa kuhusu upimaji wa afya kwa hiari na matumizi sahihi ya njia za kujikinga na maambukizi ya Virusi vya UKIMWI pamoja na kuendelea kushirikiana kwa karibu na mashirika na wadau wa afya ili kuboresha huduma za kinga na tiba,” alisema Elikana

Naye Mganga Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Dkt. Kheri Kagya, akiwasilisha taarifa ya hali ya UKIMWI mkoani humo, amesema Mkoa wa Mwanza una kiwango cha maambukizi ya VVU cha asilimia 4.7, ikilinganishwa na kiwango cha kitaifa cha asilimia 4.4, kwa mujibu wa matokeo ya Utafiti wa Kitaifa wa THIS 2022/2023.

Alisema kwa mujibu wa taarifa ya DHIS2 Annual Report ya mwaka 2025/2026, Mkoa wa Mwanza unakadiriwa kuwa na idadi ya watu wanaoishi na VVU (WAVIU) 112,685.

“Mkoa, kwa kushirikiana na wadau, umeendelea kutoa elimu ya kujikinga dhidi ya maambukizi ya VVU kwa kuhamasisha matumizi sahihi ya kondomu. Katika kipindi cha mwaka 2025/2026, Mkoa ulisambaza jumla ya kondomu 2,265,772 katika jamii, hususani sehemu za kulala wageni, sehemu za kuuzia vileo (baa), kumbi za starehe na kwenye mikusanyiko mbalimbali,” alisema.






Harambee ya kuchangisha fedha na vifaa kwa ajili ya kuendeleza ujenzi wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Kaskazini, Jimbo la Kilimanjaro, kupitia Usharika wa Msitu wa Tembo, Mtaa wa Israel, imefanyika kwa mafanikio huku viongozi na wadau mbalimbali wakijitokeza kuunga mkono ujenzi huo.

Katika harambee hiyo, Mdau wa maendeleo wilayani Simanjiro, Taiko Ole Kulunju, ameendelea kuonesha mshikamano wake katika kusaidia shughuli za maendeleo kwa kuchangia kiasi cha shilingi milioni 4 pamoja na mifuko 100 ya saruji, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuhakikisha ujenzi wa jengo hilo unakamilika.

Taiko Ole Kulunju amesema mchango wake ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za waumini na uongozi wa kanisa katika kuhakikisha wanapata jengo lenye mazingira bora kwa ajili ya ibada pamoja na shughuli mbalimbali za kijamii.

Amesisitiza kuwa maendeleo hayawezi kufikiwa na mtu mmoja pekee, bali yanahitaji ushirikiano wa viongozi, taasisi za dini, wafanyabiashara, wadau wa maendeleo na wananchi kwa ujumla, bila kujali tofauti zao.

Harambee hiyo pia imehudhuriwa na viongozi mbalimbali wa serikali, akiwemo Frank Ole Leshwa, mwakilishi wa Mbunge wa Jimbo la Simanjiro, Mhe. James Ole Milya, pamoja na madiwani mbalimbali kutoka Wilaya ya Simanjiro. Kwa pamoja, viongozi hao wamechangia zaidi ya shilingi milioni 21, ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za waumini katika kukamilisha ujenzi wa kanisa hilo.

Kwa upande wake, Diwani mwenyeji na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro, Mh Kaleya Mollel, ambaye alikuwa mgeni rasmi katika harambee hiyo, amewashukuru viongozi, waumini na wadau wote waliojitokeza kuchangia ujenzi huo kwa fedha, vifaa na namna nyingine mbalimbali.

Mhe. Kaleya amesema ushirikiano na moyo wa kujitolea uliooneshwa na washiriki wa harambee hiyo ni mfano mzuri wa mshikamano unaopaswa kuendelezwa katika jamii, hususan katika kusaidia miradi yenye manufaa kwa wananchi.

Lengo la harambee hiyo ni kuchangisha fedha na vifaa kwa ajili ya kuendeleza ujenzi wa jengo la kanisa, ikiwemo kukamilisha hatua mbalimbali za ujenzi kutoka kwenye lenta ya kwanza na ya pili hadi hatua ya upauaji, pamoja na mahitaji mengine muhimu.

Mchango wa Taiko Ole Kulunju na viongozi wengine katika harambee hii unaonesha kuwa maendeleo ya jamii hayapaswi kubaki kuwa jukumu la taasisi au kundi moja pekee. 

Pale viongozi, taasisi za dini, wafanyabiashara na wananchi wanapoweka tofauti zao pembeni na kuungana kwa lengo moja, miradi ya kijamii hupata nguvu na kasi ya kukamilika. 

Harambee hii ni mfano unaothibitisha kuwa mshikamano, kujitolea na uwajibikaji wa pamoja vinaweza kuwa chachu ya maendeleo endelevu katika jamii.




 Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba Nchini (TMDA), imeingia mashirikiano na Mamlaka ya Udhibiti wa Dawa ya Denmark, (Danish Medicines Agency 

-DKMA) katika nyanja ya udhibiti wa bidhaa tiba Nchini.

Hayo yamebainishwa wakati wa kikao maalum kilichofanyika Jijini Arusha hivi karibuni, ambapo ujumbe wa DKMA umekutana na uongozi wa TMDA ulioongozwa na Mkurugenzi Mkuu wake Dkt. Adam Fimbo.

Katika kikao hicho, maeneo ya ushirikiano yaliyojadiliwa ni pamoja na matumizi ya Teknolojia ya Akili Unde 'AI' katika udhibiti wa vifaa tiba, ufuatiliaji wa ubora na usalama wa bidhaa tiba pamoja na usugu wa vimelea vya magonjwa dhidi ya dawa.

Wakizungumza baada ya kikao hicho, pande zote mbili zimesema ushirikiano huo utasaidia kubadilishana uzoefu, taarifa za kisayansi na kuimarisha mifumo ya udhibiti ili kuhakikisha bidhaa tiba zinazopatikana ni salama, zenye ubora na zinafaa.

Aidha, TMDA ni miongoni mwa mamlaka bora barani Afrika katika ubora wa maabara. Maabara yake imepata hadhi ya WHO Prequalified na ipo katika orodha ya maabara 57 duniani zilizothibitishwa na WHO.

Kwa upande wa DKMA ina dhamira ya kuwa kinara katika ushirikiano wa kitaifa na kimataifa na mamlaka za dawa duniani kote.






 


Na Oscar Assenga, Tanga



WAZIRI wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda, anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika uzinduzi wa Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu 2026, inayofanyika katika Viwanja vya Usagara, jijini Tanga.

Maonyesho hayo yaliyoanza Agosti 15 na yanatarajiwa kuendelea hadi Agosti 24, mwaka huu, yanalenga kuonyesha mchango wa elimu, ujuzi, sayansi, teknolojia na ubunifu katika kufikia malengo ya maendeleo ya Taifa kupitia Dira ya Taifa 2050.

Akizungumza kuhusu maandalizi ya maonyesho hayo, Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Balozi Dk Batilda Burian, alisema mkoa huo umejiandaa kikamilifu kumpokea Profesa Mkenda pamoja na washiriki wengine watakaohudhuria tukio hilo.

Dk Batilda alisema Serikali ya Mkoa imeimarisha maandalizi, ikiwemo ulinzi na usalama, ili kuhakikisha washiriki na wananchi wanaotembelea maonyesho hayo wanapata mazingira salama na rafiki.

“Tanga inajivunia kuwa mwenyeji wa maonyesho haya. Tunawahakikishia Wizara ya Elimu na wananchi kuwa Serikali ya Mkoa imejipanga kuhakikisha ulinzi na usalama unaimarishwa wakati wote wa maonyesho,” alisema.

Alisema maonyesho hayo ni fursa muhimu kwa wananchi kujionea kwa vitendo namna Serikali, taasisi za elimu, watafiti na wabunifu wanavyoshiriki katika kuleta maendeleo ya Taifa.

Kaulimbiu ya maonyesho hayo ni “Elimu, Ujuzi na Ubunifu: Njia ya Kufikia Dira ya Taifa 2050,” ambayo, kwa mujibu wa Dk Batilda, inaendana na hatua ambayo Taifa limefikia katika utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050.

Alisema kila sekta, taasisi, wizara, mkoa na halmashauri ina wajibu wa kuwaelimisha wananchi kuhusu Dira ya Taifa 2050 na nafasi yao katika kuifikia.

“Maonyesho haya yataonyesha Tanzania tunayotaka kuifikia ifikapo mwaka 2050. Taasisi za elimu, vyuo vya ufundi, taasisi za utafiti na shule zitaonyesha mchango wao katika kufikia dira hiyo,” alisema.
Washiriki zaidi ya 300

Dk Batilda alisema zaidi ya washiriki 300 kutoka maeneo mbalimbali wanashiriki katika maonyesho hayo, wakiwemo wawakilishi kutoka vyuo vikuu, taasisi za utafiti na maendeleo, vyuo vya mafunzo na ufundi stadi pamoja na taasisi binafsi zinazohusiana na sayansi na teknolojia.

Alisema washiriki hao watapata fursa ya kuonyesha bunifu, teknolojia, ujuzi na shughuli mbalimbali zinazohusiana na elimu na maendeleo ya Taifa.

Aidha, alisema maonyesho hayo yanatoa fursa muhimu kwa vijana wanaotarajia kujiunga na vyuo vikuu na taasisi nyingine za elimu kupata taarifa sahihi kuhusu fursa za elimu na namna ya kufanya maombi ya kujiunga na vyuo.

“Vijana wanaoanza mchakato wa kujiunga na vyuo vikuu Mtapata fursa ya kuelekezwa namna sahihi ya kujaza maombi na kupata taarifa nyingine muhimu kuhusu elimu ya juu,” alisema.
Sh156 bilioni elimu Tanga

Katika hatua nyingine, Dk Batilda alimshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa uwekezaji mkubwa unaofanywa katika sekta ya elimu, akisema Mkoa wa Tanga umepokea zaidi ya Sh156 bilioni kwa ajili ya kuboresha mazingira ya kujifunza na kufundishia.

Alisema uwekezaji huo ni sehemu ya juhudi za Serikali kuhakikisha wanafunzi wanapata mazingira bora ya elimu na kuongeza ubora wa huduma za elimu nchini.

Pia alimpongeza Profesa Mkenda na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa kuendelea kuunga mkono maonyesho hayo, akisema tukio hilo limeendelea kukua na kuboreshwa.

Kwa upande mwingine, Mkuu huyo wa Mkoa aliwataka wananchi wa Tanga na mikoa jirani kujitokeza kwa wingi katika Viwanja vya Usagara kushuhudia maonyesho hayo na kupata elimu kuhusu fursa mbalimbali zinazopatikana katika sekta ya elimu, ujuzi, sayansi na ubunifu.

Alisema maonyesho hayo pia yatawapa wananchi nafasi ya kujionea hatua ambazo Tanzania imepiga katika matumizi ya teknolojia, utafiti na ubunifu katika kutatua changamoto mbalimbali za jamii.

Uzinduzi rasmi wa maonyesho hayo unatarajiwa kufanyika Agosti 18, 2026, ukiongozwa na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda, huku Waziri Mkuu, Mwigulu Nchemba, akitarajiwa kuwa mgeni rasmi katika hafla ya kufunga maonyesho hayo Agosti 24.


SportPesa World Cup promotion crowns 10 winners with TZS 5 million each
SportPesa World Cup promotion crowns 10 winners with TZS 5 million each

SportPesa World Cup promotion crowns 10 winners with TZS 5 million each

Ten SportPesa Tanzania customers each won TZS 5 million in the final draw of the Twenzetu Duniani na SportPesa campaign. These ten winners shared a total prize of TZS 50 million, bringing to a conclusion to the campaign after weeks of World Cup-themed draws. Their wins highlighted how the campaign combined prize rewards with shared football moments across Dar es Salaam.

The campaign offered a total prize of TZS 100 million. SportPesa allocated half of this amount to weekly draws, while the remaining TZS 50 million was split evenly among the ten final winners. During the SportPesa World Cup promotion, eligible bettors who placed qualifying bets were automatically entered into the draw. This structure made the final draw the exciting climax of a month-long event, rather than just a single prize announcement.

Ten final-draw winners each won TZS 5 million

SportPesa held the final draw on July 20th, following the promotion’s close on July 19th. Then ten winners were confirmed, each receiving TZS 5 million, totaling TZS 50 million. This result followed the promotion’s awarding structure, which set aside half of the TZS 100 million prize pool for the final draw.

According to the promotion rules, all customers with qualifying entries were eligible for the final draw. SportPesa Tanzania managed the computerized draw and contacted winners through the phone numbers linked to their accounts. Before payment, each winner’s identity was verified, ensuring a clear and organized process from entry to prize award.

Weekly rewards built momentum before the final

The ten grand-draw winners received the largest individual prizes in a broader reward program. SportPesa set aside another TZS 50 million for weekly draws, planning to select 100 winners each week. Early draws showed that over 200 people won prizes in the first two weeks, as the weekly prize pool increased from TZS 5 million in the first week to TZS 10 million in the second.Before the final draw, weekly rewards had already built momentum, with more than 200 winners recorded in the first two weeks of the campaign.

Twenzetu Duniani na SportPesa was designed to make the World Cup more rewarding for our customers. The 10 final winners show how the campaign created real reward moments, while the weekly draws and match screenings helped fans stay connected throughout the tournament,” said SportPesa Tanzania Head of Marketing Tracy Humplick.

 

Three Dar screenings took the campaign into fan spaces

By hosting screenings at Mlimani City, Mwinjuma and Tips Bar, SportPesa moved the campaign from the betting platform into real fan spaces where supporters could watch, react and celebrate together. These events provided fans with shared spaces to watch World Cup games and linked the online promotion to live football experiences across the city.

SportPesa director Abbas Tarimba attended the Mwinjuma screening to represent the company and engage with supporters during the match. His presence was welcomed by fans at the event. These three screenings also showcased SportPesa’s larger program of football match events, which gives live match watching to community and hospitality venues and helps bring fans together for major games.

Digital rewards met Dar es Salaam’s football culture

The campaign connected two key areas. SportPesa handled qualifying entries and prize draws on its platform, while the screenings brought the brand into the shared social experience of watching football. Mlimani City provided a major commercial venue, Mwinjuma brought the events to Mwananyamala, and Tips Bar extended them to Mikocheni.

This approach helped SportPesa Tanzania keep the spotlight on the winners while staying engaged throughout the tournament. The TZS 5 million prizes gave the campaign a clear and measurable end, while the screenings allowed fans to enjoy important matches together. The campaign showed how digital access and live events can work together without overshadowing the people who won.

Conclusion

The ten winners who each received TZS 5 million became the highlight of the Twenzetu Duniani na SportPesa campaign. They shared a total of TZS 50 million, completing the TZS 100 million promotion that also rewarded weekly winners. By hosting screenings at Mlimani City, Mwinjuma, and Tips Bar, SportPesa linked the World Cup’s biggest moments to both individual winners and shared fan experiences across Dar es Salaam.

Na Mwandishi Wetu
WAZIRI Wa Elimu Sayansi Na Teknolojia Profesa Adolf Mkenda anatarajiwa kuzindua wiki ya elimu,ujuzi na ubunifu inayoendelea katika viwanja vya shule ya sekondari jijini Tanga kesho Agosti 18,2026.

Mkuu wa mkoa huo, Batilda Buriani amesema hayo alipotembelea maonesho hayo na kuongeza kuwa washiriki zaidi ya 300 wapo katika wiki hiyo ambao tayari wamepanga bunifu mbalimbali katika mabanda pamoja na kutoa elimu.

Amewahakikishia wananchi usalama na ulinzi wakati wote wa maonesho na kwamba wanakaribishwa kufika kwa wingi katika viwanja hivyo ili kujifunza kaa kuwa taasisi zote za elimu zikonkatika viwanja hivyo pamoja na taasisi za utafiti.

“Kwa muda wote wa wiki moja kuanzia Agosti 15,2026 hadi Agosti 24,2026 maadhimisho yataanza saa mbili asubuhi na kufugungwa jioni saa 12”, amesema Burian na kuongeza kuwa Waziri Mkuu,Dk Mwigulu Nchemba anatarajiwa kufunga maonesho hayo yenye kauli mbiu elimu,jjuzi,ubunifu njiabya kufikia dira ya Taifa 2050.

Batilda ameongeza kuwa washirikinkatika maonesho hayo ni pamoja na vyuo vikuu,tasisi za tafiti ,vyuo vya elimu na ufundi stad na taasisi binafsi ambazo zinahusiana na sayansi na teknolojia.

Amewataka wananchi kutembelea maonesho hayo kwa kuwa ni nafasi ya pekee kujifunza mambo mbakimbali hara kwa wale wanaotafuta vyuo na usajili.

Na Mwandishi Wetu, Tanga
MAWAZO ya ubunifu na teknolojia yanayobuniwa na wanafunzi na wahitimu wa Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA) yameelezwa kuwa ni fursa muhimu kwa vijana kujiajiri, huku yakitoa suluhisho la changamoto mbalimbali zinazowakabili wananchi.

Miongoni mwa wabunifu hao ni Calven Mwakampya, mhitimu wa TIA ambaye amebuni kifaa cha teknolojia kinachoitwa Smart Glove, kinachowezesha mawasiliano kati ya mtu mwenye uziwi na asiye na uziwi.

Mwakampya amebuni mfumo unaotumia vitufe vya alama za mawasiliano, ambapo ujumbe unaowasilishwa na mtu mwenye uziwi unaweza kubadilishwa kuwa sauti na kusikika kwa mtu asiye na uziwi, hivyo kusaidia kuondoa changamoto ya mawasiliano kati ya makundi hayo.

Akizungumza katika Maonesho ya Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu yanayoendelea katika Viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara jijini Tanga, Mwakampya alisema ubunifu huo wa kiteknolojia umemsaidia kutengeneza suluhisho la changamoto ya mawasiliano inayowakabili watu wenye uziwi.

Alisema amekuwa miongoni mwa wahitimu walionufaika na mpango wa TIA wa kukuza na kuendeleza vipaji na taaluma, jambo lililomsaidia kuboresha wazo lake na hatimaye kuanzisha kampuni.

"Nimekuwa miongoni mwa wanafunzi wanaonufaika na mpango wa TIA wa kukuza na kuendeleza vipaji na taaluma, jambo linalonisaidia kuendeleza wazo ambalo sasa tumeanzisha kampuni," alisema Mwakampya.

Alisema TIA imekuwa ikimpa mwongozo na usimamizi katika kuboresha ubunifu huo, ambao umeanza kuwa suluhisho la changamoto zinazowakabili watu wenye uziwi katika mawasiliano.

Kwa mujibu wa Mwakampya, mfumo huo utamwezesha mtu mwenye uziwi kuwasiliana na mtu asiye na uziwi kwa urahisi, huku ujumbe wa alama ukibadilishwa kuwa sauti ili kumwezesha mtu asiye na uziwi kuelewa mahitaji ya anayewasiliana naye.

Alisema mfumo huo pia utasaidia kuongeza ufanisi wa mawasiliano kati ya jamii ya watu wenye uziwi na wasio na uziwi katika maeneo mbalimbali ya huduma za kijamii.

Mwakampya alisema matumizi ya teknolojia katika sekta ya mawasiliano ni muhimu katika kuhakikisha watu wenye uziwi wanapata na kutoa huduma kwa ufanisi kama ilivyo kwa watu wasio na uziwi.

Aidha, alisema mpango wa TIA wa kuendeleza mawazo na ubunifu wa wanafunzi una nafasi kubwa katika kuongeza fursa za ajira, hususani kwa vijana wanaohitimu katika vyuo mbalimbali.

"Ubunifu unaotokana na wanafunzi unaweza kuwa chanzo cha kujiajiri na pia kutoa suluhisho la changamoto mbalimbali zinazolikabili Taifa," alisema.

Alitoa wito kwa vijana kutumia maarifa wanayopata vyuoni kubuni teknolojia na bidhaa zitakazokuwa na manufaa kwa jamii, badala ya kutegemea ajira baada ya kumaliza masomo.

"Ninatoa wito kwa vijana kutumia maarifa wanayopata vyuoni kubuni teknolojia zitakazokuwa na manufaa kwa jamii," alisema Mwakampya.

Alisema miongoni mwa wadau wanaoweza kunufaika na teknolojia hiyo ni TIA kwa ajili ya kusaidia katika ufundishaji wa watu wenye uziwi, Chama cha Viziwi Tanzania (CHAVITA), hospitali na maeneo mengine ya kutolea huduma.

Na Mwandishi Wetu, Tanga
MAMLAKA ya Elimu Tanzania (TEA) imesema mkondo wa Amali katika shule za sekondari umeendelea kupata mwitikio mkubwa kutoka kwa wanafunzi kutokana na upatikanaji wa vifaa vinavyowawezesha kujifunza kwa vitendo.

Akizungumza katika Maonesho ya Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu yanayoendelea katika Viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara jijini Tanga, Afisa Miradi wa TEA, Kabula Julu, alisema shule zilizofadhiliwa vifaa kwa ajili ya mkondo wa Amali zimeanza kushuhudia ongezeko la hamasa miongoni mwa wanafunzi.

Alisema miongoni mwa shule zilizonufaika na ufadhili huo ni Shule ya Sekondari ya Wasichana Korogwe, ambayo imepatiwa vifaa vyenye thamani ya zaidi ya Sh milioni 400 kwa ajili ya kufundishia fani tano.

Alizitaja fani hizo kuwa ni Upishi, Kilimo cha Mboga na Matunda, Ushonaji, Kilimo cha Mazao ya Chakula pamoja na Afya ya Wanyama.

Julu alisema shule nyingine zilizonufaika na ufadhili wa TEA ni pamoja na Uwemba, Iringa, Kigoma, Dar es Salaam, Arusha, Chief Salwart ,Morongo pamoja na Korogwe.

Alisema miongoni mwa shughuli zinazotekelezwa na TEA ni kufadhili shule zenye mkondo wa Amali, ambao umekuwa ukipata mwitikio mkubwa kutokana na kuwawezesha wanafunzi kujifunza kwa vitendo zaidi badala ya kutegemea nadharia pekee.

"Tumefadhili shule zenye mkondo wa Amali na mwitikio umekuwa mkubwa, kwa sababu wanafunzi wana uhitaji wa kujifunza kwa vitendo zaidi kuliko nadharia," alisema Julu.

Aliongeza kuwa ushiriki wa TEA katika maonesho hayo unatoa fursa kwa wananchi kufahamu namna Mamlaka hiyo inavyoshiriki kuboresha mazingira ya elimu na kuwawezesha wanafunzi kupata ujuzi unaoweza kuwasaidia katika maisha na kujiajiri.

Kwa upande wake, Mwalimu wa Shule ya Sekondari ya Wasichana Korogwe, Catherine Machugu, alisema ufadhili wa TEA umeongeza chachu kwa wanafunzi kupenda na kusoma mkondo wa Amali.

Alisema kabla ya shule hiyo kupata vifaa, wanafunzi walikuwa wakijifunza zaidi kwa nadharia, lakini baada ya kupata vifaa wameanza kujifunza kwa vitendo na matokeo yameanza kuonekana.

"Wakati tulipokuwa hatuna vifaa, wanafunzi walijifunza zaidi kwa nadharia, lakini kwa sasa wanajifunza kwa vitendo na matokeo yanaonekana," alisema Machugu.






MRADI wa Mafunzo ya Kitaaluma ya Ufundi Stadi katika Sekta ya Migodi (IMTT) umeendelea kuwa daraja muhimu kwa vijana kupata ujuzi unaohitajika katika sekta ya migodi, huku mfumo wake wa Uanagenzi ukiwawezesha wanafunzi kujifunza darasani na kufanya kazi za vitendo katika migodi, hatua inayochangia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 ya kujenga uchumi jumuishi unaoshirikisha wananchi katika shughuli za uzalishaji.

Akizungumza na Michuzi TV katika Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu inayoendelea jijini Tanga kuanzia Agosti 15 hadi 24, Mkufunzi na Mratibu wa Uanagenzi wa IMTT kutoka VETA Moshi, mkoani Kilimanjaro, Mwl. John Nathan, amesema mpango huo ulianzishwa kwa ushirikiano kati ya VETA na Chemba ya Migodi Tanzania yaani (TCM).

Amebainisha kuwa tofauti na mafunzo ya kawaida ya darasani, mradi wa IMTT unafanyika katika mazingira mawili muhimu ni chuoni na katika eneo la kazi kwa maana ya viwandani, na Mfumo huo unamwezesha mwanafunzi kupata maarifa ya kinadharia na ujuzi wa vitendo kwa wakati mmoja, hivyo anapohitimu huwa tayari ana uzoefu wa mazingira halisi ya kazi.

“Anapokwenda kwenye kazi, anakuwa si mgeni tena, hahitaji uzoefu mwingine wa ziada ili kukidhi mahitaji ya ajira kwa sababu tayari ana uzoefu uliojengwa kutokana na muundo wa mafunzo".

Amesema kwa sasa, IMTT inatolewa katika chuo cha VETA Moshi peke yake, hii ni baada ya tafiti za awali zilifanyika na kubaini kuwa chuo hicho kilikuwa na mazingira, vifaa na miundombinu iliyohitajika kuendesha mafunzo hayo. Hata hivyo baadhi ya kampuni za migodi zimekuwa zikisaidia vijana kutoka maeneo yanayozunguka migodi kusafiri hadi Moshi kwa ajili ya mafunzo kabla ya kurejea katika maeneo yao ya kazi.

Ameeleza kuwa kwa mtu yeyote anayehitaji kujiunga na IMTT anatakiwa kuwa na ufaulu wa Kidato cha Nne na kuwa mzawa wa Tanzania na taarifa zaidi kuhusu taratibu za kujiunga wanaweza kufika VETA Moshi au kupata taarifa kupitia tovuti ya VETA.

Kwa upande wa mafanikio, amesema zaidi ya vijana 1,668 wamepatiwa mafunzo kupitia IMTT tangu kuanzishwa kwake mwaka 2009, ambapo asilimia 79.1 wameajiriwa katika migodi mbalimbali nchini, huku asilimia 1.1 wamepata ajira katika migodi nje ya nchi hali inayoonesha kuwa mafunzo ya ufundi stadi yanaweza kuwa njia muhimu ya kuwawezesha vijana kupata ajira.

Akieleza mchango wa programu hiyo katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, amesema IMTT inawawezesha vijana kushiriki moja kwa moja katika sekta ya migodi kwa kuwapatia ujuzi unaowawezesha kuwa sehemu ya nguvu kazi yenye tija, ambapo ajira wanazopata vijana hao haziwanufaishi wao pekee, bali pia familia zao na jamii zinazowazunguka.

Aidha, amegusia mabadiliko ya teknolojia katika sekta ya migodi yameifanya VETA kuendelea kuboresha mitaala ili kukidhi mahitaji mapya, hususan katika uchimbaji wa chini ya ardhi, amesema wanatarajia kuja na Programu sita mpya ambazo ni Scoop Operation, Tele-remote Bogger Operation, Cubex Operation, Jumbo Operation, Lifting and Rigging pamoja na Mobile Charging Unit Operation ili kuongeza ujuzi wa vijana wataokwenda kuisaidia sekta ya migodi kikamilifu kulingana na kasi ya ukuaji wa teknolojia.

Akitoa ujumbe kwa vijana wanaotembelea Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu inayofanyika katika viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara jijini Tanga, aliwataka kutumia fursa hiyo kupata taarifa kuhusu mafunzo ya ufundi stadi na kuchukua hatua badala ya kubaki na ndoto bila kuzifanyia kazi.

“Usiwe na wazo kichwani ukabaki na wazo, fanyia kazi, anza sasa,” akieleza kuwa vijana waliopitia IMTT wameweza kufikia fursa mbalimbali za ajira ndani na nje ya nchi, jambo linaloonesha kuwa ujuzi wa ufundi unaweza kuwa msingi wa mafanikio ya kiuchumi kwa vijana.




Na Mwandishi Wetu
JUMUIYA ya Wanawake katika Nyuklia Tanzania (WiNTz) imetembelea Hospitali ya KCMC na kufanya mazungumzo na wanawake wanaofanya kazi katika Kitengo cha Tiba ya Mionzi, ikiwa ni sehemu ya juhudi za Jumuiya hiyo kuwawezesha wanawake katika sekta ya sayansi na teknolojia ya nyuklia kupata fursa za masomo na mafunzo ya muda mfupi na muda mrefu ndani na nje ya nchi.

Ziara hiyo imelenga pia kuwajengea uwezo wanawake wanaofanya kazi katika eneo la tiba ya mionzi kwa kuwafungulia fursa mbalimbali za kitaaluma zitakazowawezesha kuongeza maarifa na ujuzi katika taaluma zao na hivyo kuboresha zaidi huduma wanazozitoa kwa wananchi.

WiNTz, inayoongozwa na Rais wake ambaye pia ni Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania (TAEC), Prof. Najat Kassim Mohammed, imeendelea kutekeleza programu mbalimbali zinazolenga kuongeza ushiriki wa wanawake na wasichana katika sayansi na teknolojia ya nyuklia nchini.

Miongoni mwa maeneo ambayo Jumuiya hiyo imekuwa ikiyapa kipaumbele ni kuhamasisha wasichana kusoma masomo ya sayansi, kutoa elimu kwa jamii kuhusu umuhimu wa uchunguzi wa saratani mapema, pamoja na kuwaunganisha wanawake wanaosoma na kufanya kazi katika taaluma za sayansi na fursa za masomo, tafiti na mafunzo ya kitaaluma ndani na nje ya Tanzania.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mkaguzi wa Vyanzo vya Mionzi kutoka Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania (TAEC), Bi. Lucy Lway, amesema pamoja na kukutana na wanawake wanaofanya kazi katika Kitengo cha Tiba ya Mionzi, WiNTz imetumia ziara hiyo kuwafariji watoto wanaopata matibabu ya saratani katika Hospitali ya KCMC.

Amesema Jumuiya hiyo inaamini kuwa pamoja na kuendeleza taaluma na kuwajengea uwezo wanawake katika sekta ya nyuklia, ni muhimu pia kutumia nafasi hiyo kuigusa jamii, hususan wagonjwa wanaopitia vipindi virefu vya matibabu.

Kwa upande wake, Mtaalamu wa Maabara kutoka TAEC, Bi. Hellen Kiyengo, amesema kujenga uelewa sahihi kuhusu teknolojia ya nyuklia ni muhimu katika kuisaidia jamii kufahamu matumizi na manufaa yake katika maisha ya kila siku, ikiwemo nafasi yake katika sekta ya afya.

Amesema elimu sahihi inasaidia pia kuondoa dhana potofu kuhusu teknolojia ya nyuklia na kuwajengea wananchi uelewa wa umuhimu wa kuzingatia usalama wakati wa matumizi ya mionzi.

Naye Msimamizi wa Wodi ya Watoto wanaopata matibabu ya saratani katika Hospitali ya KCMC, Bwn. Robert Kessy, ameipongeza WiNTz kwa kutenga muda wa kuwatembelea watoto wanaopata matibabu ya saratani, akisema baadhi yao hulazimika kukaa hospitalini kwa muda mrefu kutokana na aina na hatua mbalimbali za matibabu wanayopatiwa.

Amesema kutembelewa na kupata faraja kutoka kwa watu na taasisi mbalimbali kunasaidia kuwapa moyo watoto hao pamoja na wazazi na walezi wao katika kipindi cha matibabu.

“Watoto hawa wanakaa hospitalini kwa muda mrefu wakipatiwa matibabu. Kitendo cha Jumuiya ya Wanawake katika Nyuklia Tanzania kutenga muda na kuja kuwaona ni jambo jema kwa sababu kinawapa moyo watoto pamoja na wazazi wao,” amesema Kessy.

Kwa upande wake, Daktari kutoka Kitengo cha Tiba ya Mionzi KCMC, Dkt. Vaileth Mteta, ameishukuru WiNTz kwa kukutana na wanawake wanaofanya kazi katika kitengo hicho, akisema hatua hiyo imewapa nafasi ya kufahamu zaidi kuhusu Jumuiya hiyo pamoja na fursa zinazoweza kupatikana kupitia mtandao wa wanawake wanaofanya kazi katika maeneo ya sayansi na teknolojia ya nyuklia.

Amesema mkutano huo umeongeza pia hamasa ya kuendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa uchunguzi wa saratani mapema na kuwahi kupata matibabu kabla ugonjwa haujaenea na kufikia hatua ambazo matibabu yake yanaweza kuwa magumu zaidi.

Aidha, amesema wanawake wanaofanya kazi katika Kitengo cha Tiba ya Mionzi wamepata fursa ya kufahamu namna wanavyoweza kujiunga na WiNTz na kutumia mtandao huo kujenga mahusiano ya kitaaluma, kubadilishana uzoefu na kufikia fursa mbalimbali za mafunzo na maendeleo ya taaluma.

Ziara hiyo ni sehemu ya jitihada za WiNTz za kujenga mtandao mpana wa wanawake katika sayansi na teknolojia ya nyuklia nchini, huku ikisisitiza umuhimu wa kuwajengea uwezo wanawake waliopo katika sekta hiyo na kuandaa kizazi kipya cha wasichana wenye ari ya kusomea masomo ya sayansi.

Kupitia shughuli hizo, WiNTz inalenga kuhakikisha wanawake wanasayansi nchini hawapati tu nafasi ya kushiriki katika maendeleo ya teknolojia ya nyuklia, bali pia wanakuwa sehemu muhimu ya kutumia sayansi hiyo katika kutatua changamoto za jamii, hususan katika afya, utafiti na maendeleo ya Taifa.


Na Karama Kenyunko, Michuzi Tv
CHUO Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS) kinaandaa mpango wa kuanzisha mafunzo ya wahudumu wa huduma za dharura watakaotoa huduma ya kwanza, ikiwemo usimamizi wa ajali, kuhakikisha njia ya hewa inabaki wazi na kumstabilisha mgonjwa kabla ya kufikishwa hospitalini.

Makamu Mkuu wa MUHAS, Prof. Apollinary Kamuhabwa, amesema hayo leo Agosti 18, 2026, Dar es Salaam wakati wa uzinduzi wa kitengo maalumu cha matibabu ya meno kwa watoto wanaohitaji dawa za usingizi au ganzi, sambamba na kusainiwa kwa hati ya makubaliano (MoU) kati ya MUHAS, Chuo Kikuu cha Ankara na Shirika la Ushirikiano na Uratibu la Türkiye (TİKA).

Amesema mpango huo ni sehemu ya ushirikiano katika huduma za tiba za dharura, ambapo MUHAS imepokea gari la wagonjwa linalotumika kutoa huduma na kuwafundisha wanafunzi.

Amesema chuo hicho kinaandaa mpango wa kuanzisha mafunzo ya wahudumu wa huduma za dharura watakaotoa huduma ya kwanza, ikiwemo usimamizi wa ajali, kuhakikisha njia ya hewa inabaki wazi na kumstabilisha mgonjwa kabla ya kufikishwa hospitalini.

Alisema mpango huo ni muhimu zaidi wakati Tanzania, Kenya na Uganda zikijiandaa kwa pamoja kuandaa Fainali za AFCON 2027.

Mkurugenzi wa TİKA nchini Tanzania, Halim Ömer, amesema mpango wa kuanzisha shule ya wahudumu wa huduma za dharura utajengwa juu ya mafunzo ya kukabiliana na majanga na dharura yaliyotolewa mwaka 2024, ambapo zaidi ya madaktari 50 wa huduma za dharura walipatiwa mafunzo.

Amesema shule hiyo itasaidia kuandaa wataalamu wenye sifa na kuimarisha uwezo wa Tanzania wa kukabiliana na dharura kwa muda mrefu.

Ömer amesema TİKA imetekeleza zaidi ya miradi 350 ya ushirikiano nchini Tanzania katika sekta mbalimbali, ikiwemo elimu, kilimo, mifugo, afya, mafunzo ya ufundi, maji na usafi wa mazingira.

Kwa upande wake, Mkuu wa Chuo Kikuu cha Ankara, Prof. Dkt. Necdet Ünüvar, amesema ushirikiano katika tiba za dharura ni hatua muhimu katika kuimarisha uhusiano wa kitaaluma na kitaalamu kati ya taasisi hizo, huku akiahidi kupanua ushirikiano katika sayansi za afya.

Prof. Kamuhabwa amesema MoU iliyosainiwa haijaweka kiwango maalumu cha fedha, bali imeweka msingi wa taasisi hizo kuandaa na kutekeleza miradi ya pamoja na kutafuta fedha kutoka TİKA na washirika wengine wa maendeleo

Top News