Yawataka wananchi kujiunga mapema kujikinga na gharama za matibabu

Na Grace Michael, Dodoma

MFUKO wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) umewahimiza wananchi nchini kujiunga na bima ya afya kabla ya kuugua, ukieleza kuwa ni njia salama ya kujikinga dhidi ya gharama kubwa za matibabu ambazo zinaweza kujitokeza wakati wowote.

Wito huo umetolewa leo Agosti 07, 2026 na Meneja Masoko na Huduma kwa Wateja wa NHIF, Angela Mziray, wakati akitoa elimu kwa wananchi waliotembelea banda la Mfuko katika Maonesho ya 49 ya Kilimo ya Nanenane yanayoendelea katika viwanja vya Nzuguni, mkoani Dodoma.

Bi. Mziray amesema maonesho hayo yameipa NHIF fursa ya kuwafikia wananchi wengi na kuwaelimisha kuhusu umuhimu wa kuwa na bima ya afya, sambamba na utekelezaji wa Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote inayolenga kuhakikisha kila Mtanzania anapata huduma za matibabu bila vikwazo vya kifedha.

Amesema changamoto za kiafya zinaweza kumpata mtu yeyote bila kutarajia, na mara nyingi husababisha familia nyingi kutumia akiba zao au hata kuuza mali ili kugharamia matibabu.

“Ugonjwa huja bila taarifa. Unaweza kuwa mzima leo lakini kesho ukahitaji matibabu ya gharama kubwa. Ndiyo maana tunawahimiza wananchi kujiunga na bima ya afya mapema ili wajenge kinga ya kifedha kwao na kwa familia zao," amesema Bi. Mziray.

Amefafanua kuwa mwananchi anapochangia bima ya afya kabla hajaugua, hupata uhakika wa matibabu bila kubeba mzigo mkubwa wa gharama wakati wa uhitaji.

“Ni muhimu wananchi wajidundulize kidogo kidogo na kuchangia bima ya afya. Hii ndiyo njia bora ya kuhakikisha familia inapata huduma za matibabu kwa wakati bila kuathiri mipango ya maendeleo," amesema.

Bi. Mziray amesema NHIF inaendelea kutoa elimu katika maeneo mbalimbali nchini ili kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu faida za bima ya afya na kuhamasisha matumizi ya mfumo wa bima badala ya kulipia matibabu moja kwa moja kutoka mfukoni.

Ameongeza kuwa wanachama wa NHIF wanapata huduma katika mtandao mpana wa vituo vya afya vya Serikali, binafsi na vya mashirika ya dini vilivyosajiliwa na Mfuko, jambo linalowapa urahisi wa kupata huduma popote wanapozihitaji.

Aidha, amesema kuwa na bima ya afya siyo tu kulinda afya ya mtu binafsi, bali pia ni kulinda uchumi wa familia kwa kupunguza matumizi yasiyotarajiwa yanayotokana na matibabu.

Katika Maonesho ya Nanenane, NHIF inaendelea kutoa huduma mbalimbali ikiwemo usajili wa wanachama wapya, elimu kuhusu vifurushi vya bima ya afya, ushauri kwa wanachama pamoja na ufafanuzi wa utekelezaji wa Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote.

Wananchi wanaotembelea banda la NHIF pia wanapata fursa ya kuuliza maswali, kupata majibu kuhusu huduma za Mfuko na kujiunga na bima ya afya papo hapo, hatua inayochangia kuongeza uelewa na ushiriki wa jamii katika kuhakikisha kila Mtanzania anakuwa na kinga ya kifedha dhidi ya gharama za matibabu.
Kaimu Katibu Mkuu wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT) Mwl. Protas Magesa amefanya kikao maalum na watumishi wastaafu wa CWT, ikiwa ni kuthamini mchango wa waasisi na watumishi wastaafu wa chama waliowahi kutumikia kwa nyadhifa mbalimbali.

Kikao hicho kimefanyika leo katika Ukumbi wa Royal Village, jijini Dodoma, kikiongozwa na Kaimu Katibu Mkuu wa CWT, Mwl. Magesa Protas Magesa, akiambatana na Kaimu Mwekahazina wa CWT, Mwl. James Asagwile, pamoja na viongozi wa CWT Mkoa wa Dodoma.

Chama cha Walimu Tanzania, CWT, kimeendelea kuthibitisha dhamira yake ya kuthamini mchango wa watumishi wastaafu kwa lengo la kusikiliza ushauri, maoni na uzoefu wao kiutendaji kuhusu mustakabali wa chama na namna bora ya kuendelea kukijenga ili kiweze kuwahudumia wanachama kwa ufanisi zaidi.

Akizungumza katika kikao hicho, Mwl. Magesa amesema uongozi wa sasa unaamini kuwa uzoefu wa watumishi wastaafu ni hazina muhimu katika kuimarisha utendaji wa chama na miongoni mwa vipaumbele vya uongozi wake ni kuboresha huduma kwa wanachama na kutatua changamoto zilizodumu kwa muda mrefu, ikiwemo kuanza kulipa madeni ya mkono wa kwaheri pamoja na mabati kwa wastaafu.

Mwl. Magesa amesisitiza kuwa anatambua mchango mkubwa wa watumishi hao, wengi wao wakiwa sehemu ya waasisi walioijenga CWT tangu kuanzishwa kwake zaidi ya miaka 30 iliyopita na ameahidi kuendeleza maono yao kwa kuhakikisha chama kinaendelea kuwa imara, chenye mshikamano na kinachotetea maslahi ya walimu kwa ufanisi pia ni sehemu ya juhudi za uongozi wa CWT .

Kwa upande wake, Kaimu Mwekahazina wa CWT, Mwl. James Asagwile, amesema waasisi wa chama wameweka msingi imara uliowezesha kuzalisha viongozi wengi wanaoendelea kulitumikia taifa kupitia CWT. pia mebainisha kuwa uongozi wa sasa utaendelea kusikiliza ushauri wao na kwamba uzoefu wa watumishi wastaafu ni nguzo muhimu katika kuendelea kuijenga CWT.

Akizungumza kwa niaba ya watumishi wastaafu, Mwl. Dauda Bilikesi ameishukuru Ofisi ya Katibu Mkuu kwa kuandaa kikao hicho, akisema hatua hiyo imeonesha kuthamini mchango wa waliolitumikia chama kwa miaka mingi na kwasasa wastaafu wana matumaini makubwa ya kuona CWT ikiendelea kukua na kuimarisha nafasi yake katika kutetea na kuzungumzia maslahi ya walimu nchini.





Na Janeth Raphael - MichuziTv 

Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) imesema Serikali inaendelea kuweka mazingira wezeshi kwa wabunifu vijana nchini kwa kuwawezesha kupata mitaji, kulinda haki zao za ubunifu na kuwaunganisha na taasisi mbalimbali ili bunifu zao ziweze kufikia hatua ya kibiashara na kuchangia maendeleo ya uchumi wa taifa.

Mkurugenzi Mkuu wa COSTECH, Dkt Amos Nungu, amesema hayo baada ya kutembelea Banda la Vijana linaloshirikisha washiriki wa Programu ya Jenga Kesho iliyo Bora (BBT) katika Maonesho ya Kitaifa na Kimataifa ya Kilimo (Nanenane) yanayoendelea katika Viwanja vya Dk. John Samwel Malecela, Nzuguni jijini Dodoma, ambapo alipata fursa ya kukutana na wabunifu waliopo ndani na nje ya programu hiyo na kusikiliza changamoto zinazowakabili.

Dkt. Nungu amesema COSTECH imeweka mifumo mbalimbali ya kuwawezesha wabunifu, ikiwemo utoaji wa fedha za kukuza bunifu (seed funding), dhamana za mikopo (guarantee schemes) pamoja na kuwaunganisha na taasisi nyingine zinazoweza kuwasaidia kupata mitaji na fursa za kupeleka bidhaa zao sokoni. 

Hata hivyo, amesema bado vijana hao wanakabiliwa na changamoto zinazohusisha usajili wa kampuni, utambulisho wa bidhaa zao na upatikanaji wa vibali mbalimbali, hivyo COSTECH imeanza kushirikiana na wadau husika kutafuta suluhisho la changamoto hizo.

Amesema kikao hicho kilihusisha pia Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI), Wakala wa Mbolea na taasisi nyingine zinazohusika na sekta ya kilimo na ubunifu, huku akieleza kuwa maoni yaliyotolewa na vijana yamepokelewa na yatafanyiwa kazi kwa kushirikiana na mamlaka husika.

Kwa mujibu wa Dkt Nungu, moja ya maeneo yaliyopewa kipaumbele ni ulinzi wa haki miliki za wabunifu, akisisitiza kuwa ubunifu unapaswa kulindwa ili uweze kuwa na tija kwa mbunifu na taifa kwa ujumla. 

Ametoa mfano wa kijana aliyebuni teknolojia ya kutengeneza mbolea kwa kutumia nywele ambaye, baada ya kupata msaada wa COSTECH katika usajili na ulinzi wa haki zake za ubunifu, aliweza kupata uwekezaji na fedha kutoka nje ya nchi.

“Hii inaonyesha kuwa msaada wa Serikali si fedha pekee, bali pia ni kujenga mazingira rafiki yanayowezesha wabunifu kulinda kazi zao, kuziboresha na kuzifikisha sokoni,” amesema.

Aidha, Dkt Nungu amesema vijana hao wameiomba Serikali kupitia COSTECH kuangalia utaratibu wa marejesho ya mikopo inayotolewa na halmashauri, wakieleza kuwa muda wa kuanza kurejesha mikopo hiyo ni mfupi na hauwapi nafasi ya kutosha kuendeleza miradi yao kabla ya kuanza kulipa. 

Amesema COSTECH imepokea ombi hilo na italijadili kwa kushirikiana na mamlaka husika ili kuona namna bora ya kufanya mazingira ya mikopo kuwa rafiki zaidi kwa wabunifu na wajasiriamali vijana.

Amesema kikao hicho kimekuwa na mafanikio kwa kuwa kimewezesha Serikali kupata fursa ya kusikiliza changamoto za vijana moja kwa moja na kuweka mikakati ya kuendelea kuimarisha mfumo wa ubunifu, utafiti na teknolojia kwa manufaa ya vijana na maendeleo ya taifa.











Na Mwandishi Wetu, Dodoma
NAIBU  Waziri wa Viwanda na Biashara, Dennis Londo, amesema Tume ya Ushindani (FCC) ina mchango mkubwa katika kuongeza thamani ya mazao ya Watanzania kupitia utoaji wa elimu kuhusu ushindani wa haki na ulinzi wa mlaji, jambo linalowasaidia wazalishaji na wafanyabiashara kuboresha ubora wa bidhaa zao na kuongeza ushindani katika masoko ya ndani na nje ya nchi.

Londo ametoa kauli hiyo leo Agosti 7, 2026, alipotembelea banda la FCC katika Maonesho ya Kimataifa ya Kilimo ya Nanenane yanayoendelea katika Viwanja vya Dkt. John Samwel Malecela, Nzuguni jijini Dodoma.

Amesema elimu inayotolewa na FCC imeendelea kujenga uelewa kwa wananchi kuhusu umuhimu wa ushindani wa haki, ulinzi wa mlaji na kuongeza thamani ya bidhaa zinazozalishwa nchini, hatua inayochochea ukuaji wa biashara na uchumi.

Aidha, ameipongeza FCC kwa kuendelea kushirikiana na wadau mbalimbali katika kuimarisha mazingira ya biashara, akieleza kuwa juhudi hizo zinaendana na maono ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kujenga soko lenye ushindani wa haki, uwazi na fursa sawa kwa wafanyabiashara wote.

Londo ameihimiza FCC kuendelea kutumia Maonesho ya Nanenane pamoja na majukwaa mengine ya elimu ya umma kuwafikia wananchi wengi zaidi ili kuongeza uelewa kuhusu sheria za ushindani na ulinzi wa mlaji.

Amesisitiza kuwa elimu hiyo ni nyenzo muhimu katika kuongeza thamani ya mazao, kuvutia masoko mapya na kuongeza kipato cha wakulima, wafugaji, wavuvi na wajasiriamali.

Pia ametoa wito kwa makundi hayo kutumia ipasavyo elimu wanayoipata kutoka FCC kwa kuboresha uzalishaji, kuzingatia sheria za ushindani na kuepuka vitendo vinavyovuruga soko, akibainisha kuwa hatua hiyo itasaidia kujenga uchumi shindani na kuongeza mchango wa sekta za uzalishaji katika maendeleo ya taifa.



KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo imesema ina wajibu wa kuhakikisha Shirika la Uvuvi Tanzania (TAFICO) linaendelea kuimarika na kufikia malengo yaliyokusudiwa na Serikali.

Hayo yameelezwa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Deodatus Mwanyika (Mb), leo Agosti 07,2026, wakati wa ziara ya Kamati kwenye banda la TAFICO, katika Maonesho ya Nanenane yanayoendelea katika viwanja vya Dkt. John Samuel Malecela, Nzuguni jijini Dodoma.

Kamati imetembelea TAFICO kwa lengo la kujionea maendeleo ya miradi ya kimkakati inayotekelezwa na Shirika katika kuimarisha sekta ya uvuvi nchini. Akiwa katika banda la TAFICO, Mwenyekiti wa Kamati hiyo, pamoja na wajumbe wa Kamati, walipokea maelezo kuhusu utekelezaji wa miradi mbalimbali ya kimkakati na hatua zilizofikiwa, yaliyowasilishwa na Afisa Uvuvi Mwandamizi wa TAFICO, Bw. Mgalula Lyobah.

Baada ya kupokea maelezo hayo, Mhe. Mwanyika alieleza kuridhishwa na hatua zinazopigwa na Shirika katika kutekeleza dhamira ya Serikali ya kuendeleza sekta ya uvuvi wa kisasa na kuongeza mchango wake katika uchumi wa Taifa.

"TAFICO ni mtoto wetu. Ni wajibu wetu kuhakikisha linaendelea kuimarika na kufikia malengo yaliyokusudiwa na Serikali. Tunafurahishwa na hatua zinazoendelea kuchukuliwa katika utekelezaji wa miradi ya kimkakati, ambayo itaongeza tija, ajira na mchango wa sekta ya uvuvi katika maendeleo ya nchi," alisema Mhe. Mwanyika.

Kwa upande wake, Bw. Lyobah alieleza kuwa TAFICO inaendelea kutekeleza kwa ufanisi miradi ya kimkakati inayolenga kukuza uvuvi wa bahari kuu, ikiwemo ununuzi wa meli 4 ambazo ziko katika hatua ya ununuzi na kukamilika kwa ujenzi wa miundombinu wezeshi .

Kukamilika kwa miundumbinu hii kuna kwenda sambamba na kukamilika kwa ujenzi wa bandari ya uvuvi iliyojengwa na Serikali Kilwa Masoko hizi ni jitahada za Serikali katika kuleta mapinduzi katika sekta ya uvuvi nchini.

Hatua hizi zinakwenda sambamba na malengo ya Serikali ya kuendeleza uchumi wa buluu na kuhakikisha rasilimali za uvuvi zinatumika kwa manufaa ya watanzania. Alisema Bw.Mgalula

TAFICO inaendelea kutumia Maonesho ya Nanenane kama jukwaa la kutoa elimu kwa wananchi kuhusu shughuli zake, huduma mbalimbali zinazotolewa na Shirika pamoja na fursa zinazopatikana katika sekta ya uvuvi na uchumi wa buluu.

















Na Mwandishi Wetu, Mbeya
JESHI la Polisi Mkoa wa Mbeya limefanikiwa kuwakamata watuhumiwa 67 wanaotuhumiwa kujihusisha na makosa mbalimbali ya jinai katika kipindi cha mwezi Julai 2026, ikiwa ni sehemu ya jitihada zinazoendelea za kuimarisha ulinzi na usalama wa wananchi na mali zao.

Akizungumza na waandishi wa habari, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Benjamin Kuzaga, alisema mafanikio hayo yametokana na ushirikiano mzuri kati ya Jeshi la Polisi, wananchi na wadau mbalimbali wa usalama, sambamba na kuendelea kwa oparesheni na misako dhidi ya wahalifu.

Alisema watuhumiwa hao wanakabiliwa na tuhuma mbalimbali zikiwemo mauaji, kujeruhi, kubaka, kupatikana na silaha bila kibali, dawa za kulevya na wizi. Aliongeza kuwa watuhumiwa ambao upelelezi wa kesi zao umekamilika tayari wamefikishwa mahakamani, huku baadhi yao wakipatikana na hatia na kuhukumiwa vifungo.
Atiwa mbaroni kwa tuhuma za mauaji ya jirani yake

Miongoni mwa waliokamatwa ni Franko Malaika Green (35), mkazi wa Kibatata wilayani Rungwe, anayekabiliwa na tuhuma za kumuua jirani yake, Edward Nwankusye (38).

Kwa mujibu wa Kamanda Kuzaga, tukio hilo lilitokea Julai 23, 2026 katika Kijiji cha Kibatata, Kata ya Kisondela, Wilaya ya Rungwe, ambapo mtuhumiwa anadaiwa kumvamia marehemu akiwa njiani kurejea nyumbani na kumkata kwa panga kichwani na mikononi, na kumsababishia majeraha makubwa.

Marehemu alikimbizwa Hospitali ya Wilaya ya Rungwe kwa matibabu, lakini alifariki dunia muda mfupi baadaye.

Kamanda Kuzaga alisema baada ya tukio hilo, kikosi maalumu cha askari wa kuzuia na kupambana na matukio ya mauaji kilianza uchunguzi na kufanikiwa kumkamata mtuhumiwa. Uchunguzi wa awali umebaini kuwa chanzo cha tukio hilo kinahusishwa na imani za kishirikina.
Dawa za kulevya, silaha na vipodozi vilivyopigwa marufuku vyakamatwa

Katika oparesheni hizo, Jeshi la Polisi liliwakamata watuhumiwa saba waliokuwa na kilogramu 12 na gramu 829 za bangi.

Aidha, watuhumiwa watatu walikamatwa wakiwa na lita 17.5 za pombe haramu aina ya gongo, huku watuhumiwa wawili wakinaswa na maboksi 555 ya vipodozi vyenye viambata sumu vilivyopigwa marufuku nchini. Watu wengine wawili walikamatwa wakiwa na silaha aina ya gobole bila kibali.
Kesi 130 zapata hukumu

Kamanda Kuzaga alisema katika kipindi cha Julai 2026, jumla ya kesi 324 zilifikishwa mahakamani. Kati ya hizo, kesi 130 zilimalizika kwa washitakiwa kutiwa hatiani na kuhukumiwa vifungo, huku kesi 164 zikiendelea kusikilizwa katika hatua mbalimbali za mahakama.
Madereva wanane wafungiwa leseni

Katika jitihada za kupunguza ajali za barabarani, Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya limeendelea kutoa elimu ya usalama barabarani na kusimamia utekelezaji wa sheria za usalama barabarani.

Kwa kipindi hicho, madereva wanane walifungiwa leseni zao za udereva baada ya kubainika kufanya makosa hatarishi, ikiwemo kuendesha kwa mwendo kasi na kuyapita magari katika maeneo yenye kona, milima na sehemu ambazo kupita kunakatazwa.
Ulinzi wa Nanenane waimarishwa

Kamanda Kuzaga alisema Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya limejipanga kuimarisha ulinzi na usalama kuelekea Maonesho ya Nanenane ya Kanda yatakayofanyika mkoani humo.

Alisema doria zimeongezwa katika maeneo mbalimbali ili kuhakikisha wananchi na wageni watakaoshiriki maonesho hayo pamoja na watakaotembelea Viwanja vya Maonesho vya John Mwakangale wanakuwa salama.

Aidha, alitoa wito kwa wananchi kuendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi kwa kutoa taarifa za uhalifu na wahalifu pamoja na kushiriki katika elimu za kiusalama ili kuimarisha mapambano dhidi ya uhalifu.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi Profesa Gidius Kyaharara akipokea zawadi mfuko kutoka kwa Afisa Uhusiano wa Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC)  Nicholas Kinyariri wakati  wakati Katibu Mkuu huyo alipotembelea  Banda la TASAC Maonesho ya Kilimo Kimataifa yanayoendelea viwanja vya Dkt.John Samwel Malecela Nzuguni jijini Dodoma.

Na Mwandishi Wetu, Dodoma
SERIKALI imesema inaendelea kuimarisha miundombinu na huduma za usafirishaji ili kuwawezesha wakulima kusafirisha mazao yao kwa usalama na kwa wakati, hatua inayolenga kuongeza upatikanaji wa masoko na kupunguza hasara baada ya mavuno.

Kauli hiyo imetolewa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Profesa Godius Kyaharara, baada ya kutembelea mabanda ya taasisi zilizo chini ya Wizara ya Uchukuzi katika Maonesho ya Kimataifa ya Kilimo ya Nanenane yanayoendelea katika Viwanja vya Dkt. John Samwel Malecela, Nzuguni, jijini Dodoma.

Profesa Kyaharara amesema usafiri bora ni nguzo muhimu katika kuhakikisha mazao yanayozalishwa na wakulima yanafika sokoni kwa wakati na katika ubora unaotakiwa, hivyo kupunguza upotevu wa mazao na kuongeza kipato cha wazalishaji.

Amesema Serikali inaendelea kuweka mazingira salama ya usafirishaji wa mazao kwa kuwa hatua hiyo inalinda juhudi na uwekezaji wa wakulima, huku ikihakikisha mazao yanafika katika maeneo yenye uhitaji bila vikwazo visivyo vya lazima.

Aidha, amesema Serikali imeendelea kuweka mazingira wezeshi kwa upatikanaji wa mitaji na uwekezaji katika sekta ya usafirishaji, hususan kipindi cha mavuno, ili kurahisisha usafirishaji wa mazao kutoka maeneo ya uzalishaji kwenda katika masoko mbalimbali nchini.

Profesa Kyaharara amesema Serikali pia inaendelea kuboresha miundombinu ya usafiri katika maeneo ya uzalishaji ili kurahisisha usafirishaji wa mazao kutoka mashambani hadi kwenye masoko ya ndani na nje ya maeneo ya uzalishaji.

Katika hatua nyingine, amesema Serikali inaendelea kuwaunganisha wakulima na masoko ya uhakika ili kuongeza thamani ya mazao yao, kuboresha kipato na kuwahamasisha kuongeza uzalishaji.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi Profesa Gidius Kyaharara akipata maelezo kutoka kwa Afisa Uhusiano wa   Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC) Nicholas Kinyariri wakati Katbu Mkuu huyo alipotembelea Banda la TASAC Maonesho ya Kilimo Kimataifa yanayoendelea viwanja vya Dkt.John Samwel Malecela Nzuguni jijini Dodoma.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi Profesa Gidius Kyaharara akisaini kitabu katika Banda Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC) wakati alipotembelea Banda la TASAC Maonesho ya Kilimo Kimataifa yanayoendelea viwanja vya Dkt.John Samwel Malecela Nzuguni jijini Dodoma.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi Profesa Gidius Kyaharara akiwa Katika picha ya pamoja na Watumishi wa Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC)  mara baada kupata kupata maelezo ya Shirika hilo wakati kweny Maonesho ya Kilimo Kimataifa yanayoendelea viwanja vya Dkt.John Samwel Malecela Nzuguni jijini Dodoma.



Na Mwandishi Wetu
MWENYEKI wa Bodi ya Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST), Yokbeth Festo Myumbilwa, amesema tafiti za jiosayansi zinazofanywa na taasisi hiyo zina mchango mkubwa katika kuibua maeneo yenye rasilimali za madini, kuvutia uwekezaji na kuchochea ukuaji wa uchumi wa Taifa unaolengwa katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Akizungumza katika Maonesho ya Nanenane, Myumbilwa amesema jukumu kuu la GST ni kufanya tafiti za jiosayansi zinazobaini maeneo yenye madini na kutoa taarifa sahihi zitakazowezesha wawekezaji kufanya maamuzi ya kuwekeza katika sekta ya madini, hatua ambayo huongeza uzalishaji, ajira na mapato ya Serikali.

Amesema pamoja na sekta ya madini, tafiti za GST zina mchango katika sekta ya kilimo kupitia utambuzi wa madini yanayotumika kurejesha rutuba ya udongo katika maeneo yenye upungufu wa virutubisho. Ameeleza kuwa taasisi hiyo pia hufanya tafiti za kubaini maeneo yenye changamoto ya rutuba ili kuwezesha matumizi sahihi ya rasilimali hizo katika kuboresha uzalishaji wa kilimo.

Myumbilwa ameongeza kuwa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inalenga kuifikisha Tanzania katika uchumi wa kati wa juu wenye thamani ya takribani dola za Marekani trilioni moja, huku sekta ya madini ikiwa miongoni mwa sekta muhimu zitakazochangia kufikiwa kwa lengo hilo.

Amefafanua kuwa ili kufanikisha azma hiyo, GST imejikita katika kufanya tafiti za kina za jiosayansi ambazo hutoa taarifa muhimu kuhusu maeneo yenye fursa za madini, hivyo kuongeza uwekezaji na kukuza mchango wa sekta ya madini katika Pato la Taifa.

Aidha, amesisitiza kuwa Serikali imeendelea kuonesha dhamira ya kuimarisha shughuli za utafiti kwa kuanzisha mfuko maalumu wa utafiti wa madini utakaowezesha kufanyika kwa tafiti za kina katika maeneo mbalimbali nchini.

Amesema tafiti hizo zitapanua uelewa wa jiolojia ya Tanzania na kusaidia Serikali kubaini maeneo mapya yenye madini, jambo litakalohakikisha uchimbaji unaendelea hata baada ya migodi iliyopo sasa kufikia mwisho wa maisha yake.

Kwa mujibu wake, matokeo ya tafiti hizo pia yataiwezesha Serikali kutenga maeneo mahsusi kwa ajili ya wachimbaji wadogo, wa kati na wakubwa kulingana na taarifa za kisayansi zitakazopatikana, hatua itakayosaidia usimamizi bora na matumizi endelevu ya rasilimali za madini.

Bi. Myumbilwa amewasihi wananchi, wachimbaji na wadau wote wa sekta ya madini kutembelea banda la GST katika Maonesho ya Nanenane ili kujifunza kuhusu huduma mbalimbali zinazotolewa na taasisi hiyo, ikiwemo tafiti za jiosayansi, huduma za maabara, ramani za jiolojia na ushauri wa kitaalamu kuhusu sekta ya madini.



 

 

Na Mwandishi Wetu

Meneja Kanda ya Kati wa Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA), Bi. Hawa Lweno, ametoa wito kwa mafundi umeme kutembelea banda la Mamlaka hiyo katika Maonesho ya Nanenane yanayoendelea katika Viwanja vya John Malecela jijini Dodoma, ili kupata elimu kuhusu umuhimu wa kupata leseni za ufundi umeme zinazotolewa na EWURA, pamoja na utaratibu wa kuomba leseni hizo.

Amesema kuwa leseni za ufundi umeme ni muhimu katika kuhakikisha huduma za ufungaji, ukarabati na matengenezo ya mifumo ya umeme zinafanywa na mafundi wenye sifa na wanaozingatia viwango vya ubora na usalama, hivyo kupunguza ajali zinazoweza kusababishwa na kazi za umeme zisizokidhi matakwa ya kitaalamu.

“Hili linaendana sambamba na wito kwa wananchi kuhakikisha wanafanya ukaguzi wa mifumo yao ya umeme kila baada ya miaka mitano tangu mfumo huo ulipofungwa,” ameeleza.

Bi. Lweno amesema EWURA pia inatumia Maonesho ya Nanenane kutoa elimu kwa wananchi kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa Mkakati wa Taifa wa Nishati Safi ya Kupikia unaolenga kuongeza matumizi ya nishati safi kwa Watanzania.

Aidha, maeneo mengine yanayotolewa elimu ni pamoja na fursa za uwekezaji wa vituo vya mafuta katika maeneo ya vijijini, taratibu za kuwasilisha na kushughulikia malalamiko yanayohusu huduma zinazodhibitiwa na EWURA, pamoja na matumizi salama ya huduma za mafuta, umeme na gesi.

     

Mchungaji wa Makanisa ya Mlima wa Moto, Rose Mgeta akizungumza jijini Dar es Salaam leo Agosti 07, 2026 wakati wa Ibada ya Shukrani ya mwanzilishi wa shule za St. Mary’s.
Meneja wa Shule za St. Mary’s, Muta Rwakatare  akizungumza jijini Dar es Salaam leo Agosti 07, 2026 wakati wa Ibada ya Shukrani ya mwanzilishi wa shule za St. Mary’s.

Na Mwandishi Wetu
MENEJA wa Shule za St. Mary’s, Muta Rwakatare, amesema mabadiliko ya mitaala ya elimu yanayoendelea nchini yanaifanya shule hiyo kujiandaa zaidi kukidhi mahitaji mapya ya wazazi, wanafunzi na taifa kwa ujumla.

Rwakatare ameyasema hayo leo Agosti 7, 2026 wakati wa ibada ya shukrani kufuatia kifo cha Mchungaji Getrude Rwakatale ambaye alikuwa mmiliki wa shule hizo amesema mtaala wa sasa umeelekezwa zaidi katika matumizi ya teknolojia za kidijitali na ujuzi wa kiufundi, hivyo St. Mary’s imejipanga kuhakikisha wanafunzi wanapata elimu inayokwenda sambamba na mahitaji ya wakati.

“Ni kweli mtaala umebadilika. Sasa hivi uko kiufundi na kidijitali zaidi. Lakini kwa St. Mary’s tumejipanga kuhakikisha kwamba mtaala uliopo sasa, ambao umeletwa ukiwa mpya, unakidhi mahitaji ya wateja wetu ambao ni wazazi wetu,” amesema.

Amesema pamoja na masomo ya kitaaluma, shule hiyo itaendelea kuzingatia michezo, sanaa na tasnia mbalimbali katika malezi ya wanafunzi ili kukuza vipaji vyao na kuwaandaa kukabiliana na mahitaji ya jamii na taifa.

Aidha, ameiomba Serikali kuendelea kushirikiana na shule katika utekelezaji wa maboresho ya elimu, hususan katika eneo la teknolojia za kidijitali, akisema hatua hiyo itasaidia kurahisisha utoaji wa elimu na kuongeza ufanisi katika shule, ikiwamo binafsi.

“Kikubwa ni kwamba kwenye tasnia ya sasa tuko kidijitali zaidi. Kwa kutusaidia katika kuboresha mtaala huu, tunaamini elimu itakuwa nyepesi na nzuri zaidi kwa shule zote, hususan shule binafsi,” amesema.

Kwa upande wake, Mchungaji wa Makanisa ya Mlima wa Moto, Rose Mgeta, amesema mabadiliko ya mitaala yanahitaji jamii ya shule kujiandaa ipasavyo ili wanafunzi wapate elimu inayokidhi mahitaji ya sasa na ya baadaye.

Mgeta amesema Serikali inapaswa kuendelea kushirikiana na shule binafsi katika kuwezesha matumizi ya teknolojia katika elimu, huku akisisitiza umuhimu wa kuimarisha michezo, sayansi na masomo mengine yatakayowawezesha wanafunzi kuwa na ujuzi unaohitajika katika dunia ya sasa.

“Tunaiomba Serikali itusaidie katika hilo ili tujikite zaidi kwenye michezo na vilevile katika tasnia ya elimu kwa ujumla, lakini zaidi katika eneo la kidijitali. Tuwe na mtaala wa kidijitali zaidi, sayansi na masomo mengine yote ili tuweze kukidhi vigezo vya wazazi wetu,” amesema.

Licha ya hayo amesema shule hizo zinaendeleza misingi na tamaduni zilizoachwa na Askofu Mama, Getrude Rwakatare, huku akieleza kuwa uongozi wa sasa unaendelea kuthamini na kuendeleza kazi nzuri inayofanywa na viongozi wa Kanisa na taasisi za St. Mary’s, akiwamo Bishop Rose Mgeta.

“Kwa hiyo, kwa wazazi ambao bado hamjapata nafasi ya kuleta watoto wenu katika shule hizi, huu ni wakati sahihi na sehemu sahihi ya kuwapeleka watoto wenu kusoma katika shule za St. Mary’s,” amesema Mgeta

Amesema shule hizo zinaongozwa na wakurugenzi wenye hofu ya Mungu, maadili na upendo kwa watoto, jambo ambalo amesema ni muhimu katika kuhakikisha wanafunzi wanapata mazingira bora ya kujifunza na kukua.

Kwa mujibu wa Mgeta St. Mary’s inalenga kuhakikisha watoto wanapata elimu bora huku wakipewa malezi yanayowajenga kuwa na maadili mema na kuwawezesha kutumia vipaji vyao kwa manufaa yao na Taifa kwa ujumla.







Matukio mbalimbali katika picha.


Top News