Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara, Mhe. Balozi Waziri Rajab Salum, leo tarehe 16 Septemba 2026 amefanya kikao kazi na taasisi wezeshi kwa biashara ikiwemo BRELA, TISEZA, TANTRADE, FCC, TPA, TASAC, Idara ya Uhamiaji, Idara ya Kazi na Ajira kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, Wizara ya Uchukuzi pamoja na Halmashauri za Dar es Salaam na Mwanza kwa lengo la kujadili na kufanya maboresho katika utekelezaji wa katazo la biashara 15 ambazo haziruhusiwi kwa wageni nchini.

Akizungumza katika kikao hicho, Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara Mhe. Balozi Waziri alisema hatua hiyo imekuja kufuatia maoni na malalamiko kutoka kwa wadau mbalimbali, hivyo Wizara imeona umuhimu wa kuyafanyia tathmini ili kubaini maeneo yanayohitaji maboresho na kuhakikisha utekelezaji unazingatia malengo yaliyokusudiwa.

Mhe. Balozi Waziri alisema mapendekezo ya kikao na tathmini itawasilishwa kwa Waziri wa Viwanda na Biashara kwa hatua zaidi za na kutoa mwelekeo wa utekelezaji wake huku akisisitiza kuwa Serikali, kupitia Wizara inalenga kulinda na kuimarisha sekta ya biashara nchini kwa kuweka misingi imara ya kiuchumi na kujenga mazingira wezeshi yatakayowawezesha Watanzania kunufaika na fursa za biashara

Aidha, Balozi Waziri alisisitiza umuhimu wa kuzingatia utu katika utekelezaji wa katazo hilo, akibainisha kuwa pamoja na wajibu wa Serikali kusimamia na kutekeleza sheria, utekelezaji wake unapaswa kufanyika kwa kuzingatia utu na kuepusha usumbufu usio wa lazima kwa wahusika.

Baada ya kukamilika kwa tathmini na majadiliano, kikao hicho kilifikia hatua ya kupitisha mapendekezo yaliyofanyiwa maboresho, ambayo sasa yanawasilishwa kwa Waziri wa Viwanda na Biashara kwa ajili ya kutoa mwelekeo wa mwisho kuhusu hatua zinazofuata katika utekelezaji wa katazo hilo.

Hatua hiyo inalenga kuhakikisha kuwa utekelezaji wa katazo la biashara 15 unakwenda sambamba na sera, sheria na taratibu za Serikali, huku ukizingatia maslahi ya Taifa na mazingira wezeshi kwa Watanzania kushiriki kikamilifu katika shughuli za biashara.








Mbunge wa Jimbo la Chalinze, Mhe. Ridhiwani Kikwete, Septemba 14, 2026 amekabidhi magari mawili kwa Vikundi viwili vya wananchi ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuwawezesha wananchi kiuchumi kupitia mikopo yenye masharti nafuu.

Magari hayo aina ya Basi la abiria na gari ndogo ya kubebea mizigo, yamekabidhiwa kwa vikundi hivyo ili kuwawezesha kufanya shughuli za kiuchumi zitakazosaidia kuongeza kipato na kuboresha maisha ya wanakikundi pamoja na familia zao.

Akizungumza wakati wa ziara yake ameonesha kufurahishwa na mmoja kati ya waliopatiwa magari hayo ni kutoka kikundi cha watu wenye ulemavu ambaye amepatiwa gari ndogo kwajili ya kubeba mizigo Mhe. Kikwete amesema mpango huo ni sehemu ya mwendelezo wa kuwawezesha wananchi kupata mitaji na vitendea kazi ambavyo vitawasaidia kujiajiri na kuongeza kipato.

Amesema wananchi wanaopatiwa fursa hiyo wanapaswa kutumia vizuri mikopo na vitendea kazi wanavyokabidhiwa ili viweze kuleta tija na kuwasaidia kujikwamua kiuchumi.

Kwa mujibu wa Mhe. Kikwete, utaratibu huo unawawezesha wananchi kurejesha mikopo kidogo kidogo bila riba, jambo ambalo linawapa nafasi ya kuendesha shughuli zao bila kubanwa na gharama kubwa za marejesho.

Amesisitiza kuwa lengo la mpango huo si kutoa fedha pekee, bali ni kujenga uwezo wa wananchi kuwa na shughuli endelevu zitakazowawezesha kuongeza kipato na kukabiliana na changamoto za maisha.

Na Mwandishi Wetu - Arusha

Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Umma, Mhe. Jaji Mstaafu Hamisa Kalombola, ametoa wito kwa watumishi wa umma kutekeleza wajibu kwa uadilifu, uzalendo na uwajibikaji ikiwa ni pamoja na kuwahudumia wananchi kwa usawa sambamba na kuwa na maisha yenye taswira chanya katika jamii.

Mhe. Jaji (Mst) Kalombola, amesema hayo katika Kikao chake na watumishi wa Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori Tanzania (TAWIRI) kilicholenga kuwakumbusha kuhusu haki, wajibu, maadili na misingi ya Utumishi wa Umma ambapo amesisitiza haki kuendana na wajibu

“utumishi wa umma hauishi ofisini, nendeni mkaiwakilishe vyema serikali kwenye utoaji wa huduma na maisha mnayoishi kwenye jamii’’ amehimiza Mhe. Jaji (Mst) Kalombola.

Kwa upande wake, Katibu wa Tume ya Utumishi wa Umma, Bw. Nolasco Kipanda, ameeleza Tume hiyo katika kuhakikisha sheria, kanuni, taratibu na misingi ya Utumishi wa Umma inazingatiwa kwenye mashirika na taasisi za umma inafanya ukaguzi ambapo hadi sasa umeyafikia mashirika na taasisi 90.

Mkurugenzi Mkuu TAWIRI, Dkt. Eblate Mjingo ameeleza taasisi hiyo inatambua mchango wa Tume katika kusimamia haki za watumishi na kwamba katika ari hiyo Taasisi imewasogeza karibu watumishi kwa kuhakikisha kupitia vikao vya maamuzi watumishi wanauwakilishi huru kupitia Mwenyekiti wa chama cha wafanyakazi katika tawi la taasisi ni mjumbe mbali na kuwakilishwa na wasimamizi wao.

Kikao hiko kimefanyika Makao Makuu ya TAWIRI Njiro - Arusha ambapo kimewakutanisha wajumbe waliongozana na Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Umma,wajumbe wa Menejimenti ya TAWIRI na watumishi.









Na Mwandishi wetu, Ngorongoro

Ilinenwa “KATIKA MWAMBA HUU NITALIJENGA KANISA”, ndivyo walivyofanya waumini wa Parokia ya Mt. Petro Masanza Kona mkoani Simiyu ambapo baada ya kulijenga kanisa kwa umoja wao waliamua kutembelea hifadhi ya Ngorongoro kujionea uwezo wa mwenyezi Mungu katika uumbaji wa ulimwengu na vilivyomo.

Ziara hiyo imewashirikisha waumini 50 kutoka parokiani hapo wakiongozwa na mapadri wanne na frateli mmoja ikiwa na lengo la kuwawezesha waumini kufanya utalii wa ndani na kujifunza juu ya urithi wa dunia ambao upo ndani kasoko ya Ngorongoro.

Akiongoza ziara hiyo,Rev Fr. Furaha James ambaye ni Paroko wa Parokia ya Masanza alisema kwamba ziara hiyo imekuwa na umuhimu mkubwa kwa kuwa wamepata fursa ya kujifunza historia, utamaduni, mazingira na vivutio vya asili vilivyopo nchini.

“Tumekuja hapa kwa ajili ya kujifunza na kuona kile ambacho Mungu ametujalia katika nchi yetu. Naamini kuwa waumini wetu waliotembelea hapa wameongeza uelewa na watakuwa mabalozi wa kutunza na kutangaza vivutio vya utalii vilivyopo nchini kwetu” alisema Fr. Furaha

Aidha kwa upande wa WAWATA, akiwemo Bi. Flora Nkolongo walieleza kufurahishwa na ziara hiyo, wakisema kuwa imewapa nafasi ya kujifunza na kuwaona wanyama mbalimbali kama Simba, Faru, Nyati, Tembo na wengine wengi ambao ni mara yao ya kwanza kuwaona kwa karibu.

Ziara hiyo ilihitimishwa kwa kutembelea makumbushi ya Urithi ambako walipata historia ya ardhi ya Ngorongoro, volkano, wanyamapori, maendeleo ya binadamu na tamaduni za jamii zinazozunguka eneo hilo ambao ni Wamasai, Wahadzabe, Wairaqw na Wadatoga na waumini hao kuhitimisha ziara yao kwa kuamini kuwa NGORONGORO NI NYUMBANI KWA KILA KIUMBE.















Na: OWM – TAMISEMI, Lindi

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM–TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, amesema hajaridhishwa na kasi ya utekelezaji wa miradi inayotekelezwa na Mkandarasi KIKIM Contractors Limited kwa kushirikiana na mbia wake AMACO Enterprises katika Manispaa ya Lindi.

Miradi hiyo inahusisha ujenzi wa barabara zenye urefu wa kilomita 5.3, Stendi ya Mabasi Mitwero, Soko Kuu la Matopeni na Ofisi ya Mradi, inayotekelezwa na Serikali kupitia Mradi wa Ustawishaji Miji Tanzania (TACTIC).

Prof. Shemdoe ameeleza kutoridhishwa kwake na kasi ya utekelezaji wa miradi hiyo Septemba 15, 2026, mara baada ya kutembelea na kukagua ujenzi wa Stendi ya Mabasi ya Mitwero na Soko Kuu la Matopeni, ambapo alibaini kuwa utekelezaji wake umefikia asilimia 23, huku ikiwa imesalia miezi mitano kabla ya muda wa kukamilisha na kukabidhi miradi hiyo.

Akizungumza baada ya kukagua miradi hiyo, Prof. Shemdoe amemtaka Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Mhe. Adam Kighoma Malima, kuhakikisha suala la utekelezaji wa mikataba hiyo linashughulikiwa kwa mujibu wa masharti ya mikataba, ili kuharakisha utekelezaji na kuhakikisha miradi hiyo inakamilika kwa wakati.

“Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa, hawa wanaotukwamisha ni wakandarasi wazawa ambao usipowapa kazi wanalalamika. Hivyo, Mheshimiwa RC, hawa wana mikataba, shughulikia suala hili kwa mujibu wa mkataba, kwani wakandarasi hawa wanaonekana ni wababaishaji,” amesema Prof. Shemdoe.

Aidha, Prof. Shemdoe amemtaka Mkuu wa Mkoa wa Lindi kukutana na wakandarasi hao ili wampe mpango mkakati wa kukamilisha miradi hiyo haraka iwezekanavyo, na kuwasilisha kwake mpango kazi huo ifikapo Septemba 23, 2026.Vilevile, ameelekeza kuwa kila baada ya wiki mbili apatiwe mrejesho wa utekelezaji wa mpango huo, ili kufahamu hatua zinazochukuliwa na maendeleo ya miradi hiyo.

Akieleza chanzo cha kasi ndogo ya utekelezaji wa miradi hiyo, Mwakilishi wa Mhandisi Mshauri kutoka kampuni ya Interconsult Ltd, ambaye pia ni Mhandisi Mkazi, Mhandisi Rashidi Abdallah, amesema changamoto hiyo imetokana na mkandarasi kutokuwa amejipanga vyema kiutendaji, kutokuwa na rasilimaliwatu ya kutosha na kutumia vibaya fedha za awali alizolipwa kwa ajili ya utekelezaji wa mradi.

Naye mmoja wa Wakurugenzi wa kampuni zilizopewa kandarasi hizo, John Daniel, amekiri kuwa wamechelewa kutekeleza miradi hiyo kutokana na uzembe, huku akieleza kuwa wamejipanga kufanya kazi usiku na mchana baada ya kuzifanyia kazi changamoto zilizokuwa zikikwamisha utekelezaji.

Bw. Daniel ameomba kukutana na Mkuu wa Mkoa wa Lindi ili kuwasilisha mpango kazi wao, huku akimuomba Mkuu wa Mkoa kuwawekea malengo ya muda mfupi yatakayowawezesha kukamilisha kandarasi yao kwa wakati.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Mhe. Adam Kighoma Malima, amesema atakutana na wakandarasi hao ili wamueleze mkakati wanaokuja nao wa kukamilisha miradi yote ndani ya miezi mitano iliyobaki.

Mhe. Malima amewataka wakandarasi hao, wakati wa kikao hicho, kuwa tayari kuridhia kutoa mkataba mdogo (sub-contract) kwa mkandarasi mwingine kutekeleza sehemu ya mradi endapo wataona hawana uwezo wa kuikamilisha kwa wakati.

Katika ziara yake ya Septemba 15, 2026, Prof. Shemdoe alitembelea na kukagua pia utekelezaji wa miradi ya ujenzi wa Daraja la Ng’uni katika Kata ya Nanganga, ujenzi wa shule mpya ya msingi eneo la Shule ya Sekondari Kitandi, ujenzi wa Kituo cha Afya Chiola Nachingwea, pamoja na kufanya mkutano wa hadhara katika Kijiji cha Mtuha, Nachingwea DC.









RIYADH, SAUDI ARABIA:

Tanzania imesisitiza umuhimu wa kujenga na kutumia akili unde (Artificial Intelligence – AI) inayozingatia lugha, utamaduni, mazingira na mahitaji ya jamii, huku ikieleza dhamira ya kuimarisha uwezo wa ndani wa nchi katika teknolojia hiyo na kuongeza nafasi ya Kiswahili katika ulimwengu wa akili unde.

Msisitizo huo umetolewa katika Jukwaa la Nne la Kimataifa la UNESCO la Maadili ya Akili Unde linalofanyika mjini Riyadh, Saudi Arabia, ambapo Tanzania imeshiriki katika mjadala wa kimataifa kuhusu hatua za vitendo zinazoweza kuchukuliwa na nchi ili kuhakikisha maendeleo ya akili unde yanaenda sambamba na maadili, uwajibikaji, usalama na maendeleo jumuishi.

Katika mchango wake kwenye mjadala huo, mwakilishi wa Tanzania aliishukuru UNESCO na Serikali ya Saudi Arabia kwa kuandaa jukwaa hilo, akieleza kuwa majadiliano hayo yana umuhimu mkubwa katika kuzipa nchi nafasi ya kubadilishana uzoefu na kutafuta suluhisho la pamoja kuhusu fursa na changamoto zinazoletwa na maendeleo ya akili unde.


Aidha, Tanzania iliishukuru UNESCO kwa kuiunga mkono Serikali katika kutekeleza Mbinu ya Tathmini ya Utayari wa Akili Unde (Readiness Assessment Methodology – RAM) mwaka 2024, ambayo matokeo yake yalizinduliwa mwaka 2025.

Tathmini hiyo iliisaidia Tanzania kubaini maeneo mbalimbali yanayohitaji kuimarishwa ili kujenga mazingira wezeshi kwa maendeleo na matumizi salama, jumuishi na yenye maadili ya akili unde.

TANZANIA YASISITIZA KUJENGA UWEZO WA NDANI

Akieleza baadhi ya mapengo yaliyobainika, mwakilishi wa Tanzania alitaja umuhimu wa kuhakikisha lugha mbalimbali zinapata nafasi katika mifumo ya akili unde, akisisitiza kuwa nchi zinahitaji kujenga uwezo wa ndani ili teknolojia hiyo iweze kuakisi mazingira na mahitaji ya jamii zao.

Alieleza kuwa utegemezi mkubwa wa mifumo ya akili unde iliyotengenezwa nje unaweza kuibua changamoto zinazohusiana na uwakilishi wa tamaduni, usalama na umiliki wa data, pamoja na ulinganifu wa mifumo hiyo na sheria na maadili ya nchi husika.

Kwa msingi huo, Tanzania imeona umuhimu wa kuwekeza katika uwezo wa ndani wa kutengeneza na kutumia mifumo ya akili unde inayozingatia lugha na mazingira ya Tanzania, sambamba na kuimarisha miundombinu ya data na mifumo ya kitaifa ya usimamizi wa teknolojia hiyo.



Mwelekeo huo unaendana na hatua zinazochukuliwa na Serikali katika kuimarisha mageuzi ya kidijitali nchini. Serikali imetangaza mageuzi ya kidijitali kuwa miongoni mwa vipaumbele katika Bajeti ya mwaka 2026/2027, huku ikiendelea na maandalizi ya Mkakati wa Taifa wa Akili Unde.

KISWAHILI KUPATA NAFASI KATIKA MAPINDUZI YA AI

Moja ya hoja muhimu iliyowasilishwa na Tanzania Riyadh ni umuhimu wa kuendeleza mfumo mkubwa wa lugha (Large Language Model – LLM) wa Kiswahili, ili kuwezesha lugha hiyo kuwa sehemu muhimu ya maendeleo ya teknolojia za akili unde.

Tanzania imeeleza nia ya kushirikiana na wadau mbalimbali, wakiwemo UNESCO, katika kuendeleza mfumo huo, hatua inayolenga kuongeza uwezo wa teknolojia kuelewa na kutumia Kiswahili kwa ufasaha na kwa kuzingatia mazingira ya watumiaji wake.

Kiswahili kinachukua nafasi muhimu katika maisha ya Watanzania na ni miongoni mwa lugha zinazotumika na idadi kubwa ya watu barani Afrika. Kwa hiyo, uwekezaji katika teknolojia inayoweza kuelewa na kutumia Kiswahili una umuhimu katika kupanua ushiriki wa wananchi katika mapinduzi ya kidijitali.

Hatua hii pia inaendana na mwelekeo wa Serikali wa kuendeleza rasilimali na zana za lugha ya Kiswahili kwa ajili ya mifumo ya akili unde na uchakataji wa lugha asilia.

MAGEUZI YA KIDIJITALI KUELEKEA TANZANIA YA MAENDELEO

Mjadala wa Tanzania katika jukwaa hilo unaakisi mwelekeo mpana wa Serikali katika kutumia teknolojia za kisasa kama kichocheo cha maendeleo ya Taifa.

Katika hatua mbalimbali, Serikali imeendelea kuweka mazingira ya matumizi ya akili unde, ikiwemo kuimarisha sera na mifumo ya kidijitali, kulinda taarifa binafsi na kujenga uwezo wa rasilimali watu katika teknolojia zinazochipukia.

Mkakati wa Taifa wa Uchumi wa Kidijitali wa 2024–2034 pamoja na hatua zinazoendelea katika eneo la akili unde vinaweka msingi wa kutumia teknolojia za kisasa katika kuongeza ufanisi wa huduma, kukuza ubunifu na kuchochea shughuli za kiuchumi.

Kwa upande wa elimu, Serikali pia imeendelea kuweka msisitizo katika matumizi sahihi ya teknolojia mpya, ikiwemo akili unde, katika ufundishaji, ujifunzaji, utafiti na ujenzi wa uwezo wa walimu na wanafunzi.

TANZANIA NA AJENDA YA AI BARANI AFRIKA

Katika mjadala huo wa kimataifa, Tanzania imeendelea kuangazia pia nafasi ya Afrika katika mapinduzi ya akili unde, ikisisitiza umuhimu wa bara hilo kuongeza uwezo wake katika sayansi, teknolojia, utafiti, ubunifu na ujuzi wa kidijitali.

Kwa Tanzania, Afrika inapaswa kuwa zaidi ya mtumiaji wa teknolojia hiyo; inahitaji pia kujenga uwezo wa kuzalisha maarifa, data, mifumo na ubunifu unaozingatia mazingira ya Kiafrika.

Hii inamaanisha kuongeza uwekezaji katika wataalamu, taasisi za utafiti, miundombinu ya kidijitali na rasilimali za lugha za Kiafrika ili kuhakikisha maendeleo ya akili unde yanawanufaisha wananchi na kuchangia maendeleo ya bara.

UNESCO NA TANZANIA ZASHIRIKI KUJENGA AI YENYE MAADILI

Ushiriki wa Tanzania katika jukwaa la Riyadh unaendelea kuimarisha ushirikiano kati ya Tanzania na UNESCO katika eneo la teknolojia zinazochipukia na matumizi yake yenye uwajibikaji.

Kupitia Tathmini ya Utayari wa Akili Unde, Tanzania imepata fursa ya kutathmini mazingira yake ya kitaifa na kubaini maeneo yanayohitaji kuimarishwa katika sera, mifumo ya kitaasisi, uwezo wa watu, miundombinu na matumizi ya teknolojia hiyo.

Kwa upande mwingine, ushiriki katika mijadala ya kimataifa kama ya Riyadh unaipa Tanzania nafasi ya kushirikisha uzoefu wake, kujifunza kutoka kwa nchi nyingine na kuendelea kujenga ushirikiano wa kimataifa katika eneo la akili unde.

Hatua hizi zinaendana na dhamira ya Serikali ya kutumia mageuzi ya kidijitali, sayansi, teknolojia na ubunifu kama nyenzo za kuongeza fursa za maendeleo na kujenga Tanzania inayokwenda sambamba na mabadiliko ya kiteknolojia duniani.

TANZANIA YAANGALIA MUSTAKABALI WA TEKNOLOJIA

Kwa ujumla, ujumbe wa Tanzania katika Jukwaa la Nne la Kimataifa la UNESCO la Maadili ya Akili Unde umeweka mkazo katika kujenga teknolojia inayozingatia watu, lugha na mazingira yao.

Kupitia mjadala huo, Tanzania imeendelea kuonyesha umuhimu wa kuunganisha maendeleo ya teknolojia na mahitaji ya jamii, huku ikisisitiza kuwa akili unde inapaswa kutumika kwa kuzingatia maadili, usalama, haki, utofauti wa lugha na tamaduni, pamoja na vipaumbele vya maendeleo ya Taifa.

Ushiriki huo unaendelea kuifanya Tanzania kuwa sehemu ya mjadala wa kimataifa kuhusu mustakabali wa akili unde, wakati Serikali ikiendelea kuchukua hatua za kujenga mazingira wezeshi ya mageuzi ya kidijitali na matumizi ya teknolojia kwa maendeleo ya Taifa.

Jukwaa la Nne la Kimataifa la UNESCO la Maadili ya Akili Unde linaendelea mjini Riyadh, Saudi Arabia, likiwakutanisha viongozi, wataalamu, watafiti, watunga sera na wadau kutoka sehemu mbalimbali duniani kujadili namna ya kuimarisha ushirikiano wa kimataifa na utawala wa akili unde unaozingatia maadili na uwajibikaji.

Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba, amewasili mkoani Arusha leo Jumatano, Septemba 16, 2026, ambapo amepokelewa katika Uwanja wa Ndege wa Arusha na Mkuu wa Mkoa wa Arusha, CPA Amos Makalla, pamoja na viongozi wengine wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Serikali.

Dkt. Mwigulu yupo mkoani Arusha kwa ajili ya shughuli mbalimbali za kikazi, ikiwemo kufungua rasmi Kongamano la Kitaifa la Wanamipango, litakalofanyika kesho Alhamisi, Septemba 17, 2026, katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano Arusha (AICC).





Asasi za kiraia Zanzibar zitapata fursa ya kutumia huduma za kifedha za kidijitali kusimamia malipo, mishahara na fedha za taasisi kwa urahisi na uwazi zaidi, kufuatia makubaliano ya ushirikiano kati ya Mixx na Jukwaa la Asasi za Kiraia Zanzibar (ZANGOF).

Makubaliano hayo yatawezesha asasi zilizo chini ya ZANGOF kutumia huduma ya Mixx Business Suite kufanya malipo ya mishahara na wanufaika, pamoja na kusimamia miamala mingine ya taasisi kwa njia ya kidijitali. 

Asasi hizo pia zitaweza kupata huduma za mawasiliano na intaneti za Yas.Akizungumza katika hafla ya utiaji saini iliyofanyika leo Zanzibar, Mrajisi Mkuu wa Asasi za Kiraia Zanzibar, Ahmed Khalid Abdalla, alisema matumizi ya teknolojia yanaweza kusaidia asasi kuboresha usimamizi wa fedha na utoaji wa huduma kwa wananchi.

“Asasi za kiraia zinafanya kazi moja kwa moja na wananchi katika maeneo mbalimbali. Tunataka kuona teknolojia ikitumika kurahisisha kazi zao, kuongeza uwazi katika usimamizi wa fedha na hatimaye kuboresha huduma zinazotolewa kwa wananchi,” alisema Abdalla.

Kwa upande wake, Afisa Mtendaji Mkuu wa Mixx, Angelica Pesha, alisema ushirikiano huo utasaidia kupeleka huduma za kifedha za kidijitali karibu zaidi na asasi pamoja na jamii wanazozihudumia.

“Asasi hizi zinafanya kazi na wanawake, vijana, wajasiriamali na makundi mbalimbali katika jamii. Kupitia huduma zetu, tunataka kuwapa njia rahisi na salama zaidi za kusimamia fedha, kufanya malipo na kuweka akiba. 

Kwetu, ujumuishaji wa kifedha ni kuona huduma hizi zikimsaidia mwananchi kuboresha shughuli na maisha yake,” alisema Pesha.

Makubaliano hayo pia yanatoa fursa kwa vikundi vinavyofanya kazi na asasi za kiraia kutumia Kikoba cha Mixx, kinachowawezesha wanachama kuweka akiba, kuchangia, kununua na kuuza hisa pamoja na kukopeshana kwa njia ya kidijitali.

Mixx tayari inashirikiana na taasisi mbalimbali Zanzibar katika matumizi ya huduma za kidijitali, zikiwemo Idara ya Maendeleo ya Ushirika, ZARTSA, ZanBus na ZSTC, katika maeneo kama malipo ya wakulima, usafiri wa umma na huduma nyingine.

Makubaliano na ZANGOF yanatarajiwa kupanua matumizi ya huduma hizo kwa asasi za kiraia na vikundi vya kijamii Zanzibar.

 Afisa Mtendaji Mkuu wa Mixx Tanzania, Angelica Pesha (wa pili kulia), na Mratibu wa Jukwaa la Asasi za Kiraia Zanzibar (ZANGOF), Dkt. Mahfoudh Hassan Haji (katikati), wakionesha hati za makubaliano ya ushirikiano ambayo yatapanua upatikanaji wa huduma za kifedha za kidijitali kwa asasi za kiraia katika tukio lililofanyika leo visiwani humo.

 Wanaoshuhudia ni Mrajisi wa Asasi za Kiraia Zanzibar, Ahmed Khalid Abdalla (wa pili kushoto), Mkuu wa Yas – Zanzibar, Mohamed Waqid (kulia) na Mwenyekiti wa ZANGOF Ndugu Hassan Hamis Juma (kushoto). Kupitia ushirikiano huo, wanachama wa ZANGOF wataweza kutumia Mixx Business Suite kufanya malipo na miamala mingine ya kifedha kidijitali.

● Awasihi Watanzania kuchukua Vitambulisho vyao vya Uraia.

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, amesema Serikali kupitia Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) itaanza kuchukua hatua za kuwasajili na kuwatambua watoto walio chini ya umri wa miaka 18, ikiwa ni sehemu ya kuimarisha mfumo wa utambulisho wa Taifa.

Dkt. Mwigulu amesema hatua hiyo itamuwezesha kila Mtanzania kutambulika kuanzia hatua za mwanzo za maisha yake pamoja na kuondoa pengo lililokuwepo katika mfumo wa utambulisho kati ya mtoto anapozaliwa na anapofikisha umri wa miaka 18.

Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo leo, Jumatano, Septemba 16, 2026, wakati akiwa Mgeni Rasmi katika maadhimisho ya Siku ya Utambulisho Duniani, yaliyofanyika katika Ukumbi wa Mlimani City, Dar es Salaam.

“Mfumo huu utasaidia kupunguza usumbufu wa kutumia nyaraka au vitambulisho vingi wakati wa kupata huduma mbalimbali, kwa kuwa taarifa muhimu za mwananchi zitaendelea kutambulika na kuhifadhiwa katika mfumo mkuu wa Taifa wa utambuzi” amesema.

Aidha, Dkt. Mwigulu amewataka Watanzania ambao tayari wamesajiliwa na vitambulisho vyao vya Taifa vimekamilika kwenda kuvichukua, akisisitiza kuwa utambulisho ni msingi muhimu wa maendeleo ya mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla.

“Kitambulisho chenyewe kama nchi tumeingia gharama, tumeahirisha baadhi ya shughuli za maendeleo ili tutoe vitambulisho. Lakini tunapokuwa tumetoa kitambulisho, halafu mhusika haendi kuchukua, haya ni mambo ambayo yanakwamisha malengo mapana,” amesema.

Amesema kwa sasa NIDA imeboresha utaratibu wa kuwafahamisha wananchi pale vitambulisho vyao vinapokuwa tayari, ikiwemo kupitia ujumbe mfupi wa simu (SMS), hivyo hakuna sababu kwa wananchi waliokwishaandikishwa kuacha vitambulisho vyao kwa muda mrefu bila kuvichukua.

“Niendelee kusisitiza wananchi wote ambao wako tayari na vitambulisho vyao, basi waende kuvichukua. Lengo letu ni kuona kuwa hakuna Mtanzania anayeachwa nyuma katika kupata vitambulisho vya Taifa,” amesema.

Katika hatua nyingine, Dkt. Mwigulu amesema Serikali imeendelea kufanya maboresho katika mfumo wa utambulisho wa Taifa ili kuhakikisha unakidhi mahitaji ya sasa ya kiteknolojia, usalama wa taarifa na utoaji wa huduma kwa wananchi.

“Serikali imeendelea kuboresha mfumo wa utambulisho ili kupunguza utegemezi wa vitambulisho vingi kwa huduma mbalimbali na kuelekea katika mfumo ambao taarifa muhimu za mwananchi zinapatikana kupitia mfumo mkuu wa Taifa wa utambuzi,” amesema.

Naye, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Patrobas Katambi, amesema NIDA imefanya mapitio ya jumla ya vitambulisho vilivyotolewa katika ofisi zake na vituo 10 vya usajili vilivyopo katika kila wilaya, bila kuhusisha vituo 156 vilivyotajwa awali.

Amesema hadi sasa jumla ya watu 27,520,835 wamesajiliwa, ambapo watu 23,515,667 wamekwishapatiwa Namba za Utambulisho wa Taifa. Aidha, vitambulisho 21,526,635 vimezalishwa, huku bado kukiwa na idadi ya vitambulisho ambavyo havijachukuliwa na wananchi waliostahili kuvipata.

Kwa Upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa NIDA, James Kaji, amesema jamii inapaswa kuacha dhana kwamba NIDA ni taasisi inayotoa kadi pekee, kwa kuwa utambulisho wa Taifa ni msingi wa upatikanaji wa huduma na utambulisho wa mwananchi katika maisha yake yote.

Amesema NIDA inaendelea kuboresha kitambulisho cha Taifa ili kiwe cha kidijitali na kiweze kuhusisha taarifa muhimu za huduma mbalimbali za kijamii, ikiwemo cheti cha kuzaliwa, bima ya afya, TIN, leseni ya udereva na taarifa nyingine muhimu, huku taarifa za kiafya kama kundi la damu zikitarajiwa kusaidia wakati wa dharura, kwa kuzingatia uthibitisho wa kitabibu.

Kanji amesema usajili wa watoto tangu wanapozaliwa ni muhimu kwa sababu utamwezesha kila mtoto kutambulika na kupata huduma za kijamii kwa urahisi katika hatua zote za maisha. Amesema zoezi hilo litaanza kwa majaribio katika wilaya za Kilolo, Lungu na Kusini Unguja, kabla ya kupanuliwa katika maeneo mengine nchini.









Top News