▪️︎ Asema mapambano dhidi ya uhalifu yanahitaji mshikamano wa kimataifa

▪️︎ Aeleza teknolojia ni nyenzo muhimu katika kukabiliana na uhalifu wa kisasa


WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, amesema ushirikiano wa kikanda na kimataifa ni sharti la mafanikio katika mapambano dhidi ya uhalifu wa kimataifa unaozidi kubadilika na kuvuka mipaka.

Amesema kuwa katika dunia ya sasa, aina nyingi za uhalifu hupangwa, hufadhiliwa na kuratibiwa kwa njia za kidijitali, hali inayohitaji mifumo imara ya kiteknolojia pamoja na ushirikiano wa pamoja ili kuudhibiti kwa ufanisi.

Ametoa kauli hiyo leo Jumatatu, Mei 4, 2026, wakati akifungua rasmi Mkutano Mkuu wa 11 na Kongamano la Chama cha Waendesha Mashtaka Afrika Mashariki (EAAP), unaofanyika katika Ukumbi wa Blue Sapphire, jijini Dar es Salaam, kuanzia tarehe 4 hadi 6 Mei, 2026, wenye kaulimbiu isemayo “Matumizi ya Teknolojia katika Kukabiliana na Uhalifu Dhidi ya Wanyamapori na Uhalifu wa Kimataifa Uliopangwa.”

“Kama ambavyo uhalifu uliopangwa hauwezi kuwepo bila kuvuka mipaka, vivyo hivyo vyombo vya dola na mifumo ya haki ya jinai haviwezi kukabiliana nao kwa ufanisi bila kuwa na mifumo madhubuti ya ushirikiano wa kimataifa, hususan katika maeneo ya msaada wa kisheria na urejeshaji wa watuhumiwa,” alisema.

Akifafanua zaidi kuhusu mwelekeo wa uhalifu wa kisasa, Waziri Mkuu alisema:

“Utafiti unaonesha kuwa katika hali nyingi, uhalifu dhidi ya wanyamapori na uhalifu wa kimataifa hupangwa kidijitali, hufadhiliwa kwa njia za kielektroniki na kuratibiwa kuvuka mipaka, na pia hufichwa kwa kutumia mbinu tata za kiteknolojia, hali inayofanya mipango na athari zake kuvuka mipaka kwa kasi kubwa ambayo wakati mwingine hupita bila kugundulika.”

Alisisitiza kuwa matumizi ya teknolojia ni sehemu muhimu ya mafanikio katika mapambano hayo.

“Katika mazingira haya, hatuwezi kufanikiwa katika mapambano dhidi ya uhalifu wa kimataifa uliopangwa bila kutumia kikamilifu teknolojia kama nyenzo muhimu katika kukabiliana na changamoto hii ndani ya ukanda wa Afrika Mashariki na duniani kwa ujumla,” alisema.

Akizungumzia athari za uhalifu huo, Waziri Mkuu alisema ni tishio kwa uchumi na usalama wa mataifa.

“Ni dhahiri kwamba biashara haramu ya wanyamapori na aina nyingine za uhalifu wa kimataifa uliopangwa ni tishio kubwa kwa mataifa yetu; unachangia kupotea kwa rasilimali zetu na pia ni tishio kwa utulivu na usalama wa nchi zetu,” alisema.

Akielezea hatua zilizochukuliwa na Tanzania, Waziri Mkuu alisema Serikali imeendelea kuboresha mifumo ya kisheria ili kuimarisha ushirikiano wa kimataifa.

“Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imekuwa ikipitia na kuboresha sheria zake za msaada wa kisheria ili kupanua wigo wa ushirikiano, ikiwemo matumizi ya ushahidi wa kidijitali, ufuatiliaji wa mawasiliano na mbinu za kisasa za uchunguzi,” alisema.

Aidha, alibainisha kuwa Serikali imeondoa baadhi ya taratibu za urasimu ili kuwezesha utekelezaji wa haraka wa maombi ya msaada wa kisheria kupitia mamlaka husika.

Waziri Mkuu alizitaka nchi wanachama kutumia jukwaa la EAAP kama chombo cha kuimarisha ushirikiano wa kikanda na kubadilishana taarifa.

“Katika dunia ya sasa ambapo uhalifu hauna mipaka, majibu yetu lazima yawe ya pamoja, ya kimkakati na yenye mshikamano,” alisema.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Zainabu Katimba, alisema uwepo wa Waziri Mkuu katika mkutano huo unaonesha dhamira ya Serikali ya kuimarisha ushirikiano wa kikanda na kimataifa katika mapambano dhidi ya uhalifu.

Alisema kaulimbiu ya mkutano huo ni ya wakati muafaka na inaakisi changamoto za sasa, akiwahimiza washiriki kutumia jukwaa hilo kubadilishana uzoefu na kuimarisha mifumo ya haki katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Naye Rais wa Chama cha Waendesha Mashtaka Afrika Mashariki (EAAP), ambaye pia ni Mkurugenzi wa Mashtaka wa Jamhuri ya Kenya, Renson Ingonga, alisisitiza umuhimu wa ushirikiano na matumizi ya teknolojia katika kukabiliana na uhalifu unaobadilika kwa kasi.

Alisema mkutano huo ni fursa ya kujenga mitandao imara ya kitaaluma, kuimarisha uaminifu na kukuza mifumo ya ushirikiano itakayowezesha kukabiliana ipasavyo na uhalifu wa kimataifa uliopangwa.

Mkutano huo wa kimataifa unawakutanisha Wakurugenzi wa Mashtaka, Mawakili Wakuu wa Serikali, viongozi wa vyombo vya sheria pamoja na wadau kutoka mashirika ya kikanda na kimataifa kwa lengo la kuimarisha ushirikiano wa kimataifa na mifumo ya haki jinai katika kukabiliana na uhalifu wa kuvuka mipaka.

Chama cha Waendesha Mashtaka Afrika Mashariki (EAAP) kinaundwa na nchi wanachama ambazo ni Tanzania, Burundi, Ethiopia, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Kenya, Msumbiji, Rwanda, Seychelles, Sudan Kusini, Somalia, Malawi, Sudan, Zambia na Uganda.

Akihitimisha, Waziri Mkuu aliwataka washiriki kuhakikisha mkutano huo unazaa matokeo yenye tija kwa ukanda wa Afrika Mashariki.

“Kwa maneno hayo machache, natangaza rasmi kufunguliwa kwa Mkutano Mkuu wa 11 na Kongamano la Chama cha Waendesha Mashtaka Afrika Mashariki,” alisema.











Na Mwandishi Wetu, Dodoma

SERIKALI imeanza kuvuna matokeo ya mageuzi ya kidijitali katika sekta ya habari baada ya Waandishi wa Habari 3,357 kuthibitishwa na kupatiwa ithibati ndani ya kipindi cha chini ya mwaka mmoja kupitia mfumo wa kisasa wa TAI HABARI.

Mafanikio hayo ni hatua kubwa katika kuimarisha weledi, uwajibikaji na usimamizi wa taaluma ya uandishi wa habari nchini, kwa kuwa kwa mara ya kwanza sekta hiyo imeanza kuwa na mfumo rasmi, wa kidijitali na unaowezesha kuchakata maombi na kuhakiki waandishi wanaokidhi vigezo kwa mujibu wa sheria ya Huduma za Habari.

Akiwasilisha Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa mwaka wa fedha 2026/2027 bungeni jijini Dodoma, Waziri wa wizara hiyo, Mhe. Paul Christian Makonda, alisema kuanzia Julai 2025 hadi Aprili 2026, Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imepokea na kushughulikia jumla ya maombi 4,139 ya usajili kupitia mfumo huo wa TAI HABARI.

Kati ya maombi hayo, Waandishi wa Habari 3,357 waliokidhi vigezo vilivyoainishwa kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229, wamepatiwa ithibati.

Katika hatua nyingine, Waziri Makonda alisema JAB imeshughulikia malalamiko 14 ya uvunjifu wa maadili ya taaluma ya habari, jambo linaloonesha kuanza kuimarika kwa mfumo wa uwajibikaji katika sekta hiyo.

Aidha, Mheshimiwa Makonda alisema Serikali kupitia JAB imeandaa mwongozo maalumu wa kisheria utakaowawezesha Waandishi wa Habari wakongwe walioathiriwa na mfumo wa ithibati kureiea katika mfumo rasmi, kwa kuzingatia masharti ya Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229 ambayo ilitungwa kwa ajili ya kukuza taaluma ya uandishi wa habari.

Alisema kuwa sheria hiyo ilitungwa kwa ajili ya kukuza taaluma ya uandishi wa habari kwa kuweka mfumo wa kitaasis utakaosimamia sekta ya habari. 

“Mwongozo huu unaweka utaratibu wa kisheria wa kutambua na kuthibitisha umahiri wao kupitia tathmini maalumu ya uzoefu, weledi na maadili ya taaluma, na kuwawezesha kupata ithibati kwa mujibu wa sheria.” Alisema Mhe. Makonda

Hatua hii inalenga kulinda taaluma ya uandishi wa habari kwa kuhakikisha hata waandishi wa habari wenye uzoefu mkubwa wanapata nafasi ya kuingia katika mfumo rasmi unaotambuliwa kisheria.












Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Waziri wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Paul Christian Makonda amesema Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) kwa kushirikiana na Mfuko wa Utamaduni na Sanaa Tanzania, zitahakikisha zinawawezesha vijana wanaojiajiri katika sekta ya habari kwa kuwapa mitaji ya kukuza, kuendeleza na kuzalisha kazi zao katika ubora unaokidhi mahitaji ya soko kupitia mikopo yenye masharti nafuu.

Akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2026/2027, Mhe. Makonda amesema katika kutekeleza hilo, Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ametoa Shilingi bilioni 20 kwa ajili ya Mfuko wa Utamaduni na Sanaa, ambapo kati ya fedha hizo, Shilingi bilioni 2 tayari zimetolewa kwa ajili ya mikopo kwa Watengeneza Maudhui Mtandaoni (content creators).

Amesema fedha hizo zinalenga kuwasaidia Watengeneza Maudhui kupata vitendea kazi na kuongeza uzalishaji wa kazi zao.

Hatua hiyo inatajwa kuwa mkombozi kwa vijana wanaojiajiri katika sekta ya habari na ubunifu, kwani inafungua fursa mpya za upatikanaji wa mitaji, vifaa vya kisasa na kuongeza uzalishaji wa maudhui yenye ubora unaokidhi mahitaji ya soko la ndani na kimataifa.

“Fedha hizi zinalenga kuwawezesha Watengeneza Maudhui kupata vitendea kazi, kuboresha ubora wa kazi zao na kuongeza ushindani katika soko la kidijitali,” alisema Mhe. Makonda.

Alisema hatua hiyo inaashiria mabadiliko ya kifikra katika namna Serikali inavyotambua na kuwekeza katika kundi la vijana wabunifu, ambalo kwa muda mrefu limekuwa likikua kwa kasi bila mifumo madhubuti ya kulisimamia na kulikuza.

“Huu ni uwekezaji wa moja kwa moja katika ubunifu wa vijana na uchumi wa kidijitali, unaolenga kuongeza ajira na kipato kwa Watanzania,” aliongeza.

Kwa mujibu wa wadau wa sekta hiyo, upatikanaji wa mitaji ni changamoto kubwa inayokwamisha ukuaji wa maudhui ya kidijitali, hivyo hatua hiyo ya Serikali inatarajiwa kuongeza uzalishaji wa kazi bora, kukuza vipato na kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha ubunifu wa maudhui katika ukanda wa Afrika Mashariki. 






Halmashauri ya Jiji la Dodoma imesisitiza kuwa hakuna utoaji wa fedha unaotambuliwa katika mchakato wa kupata maeneo ya kufanyia biashara katika soko la Umonga, huku ikionya kuwa yeyote anayelipia eneo kwa sasa anakuwa ametapeliwa.

Akizungumza Mei 4, 2026, katika ukumbi wa halmashauri hiyo, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Denis Gondwe, amesema ugawaji wa maeneo kwa wafanyabiashara waliokuwa katika Soko la Rehema Nchimbi utafanyika mara baada ya kukamilika kwa taratibu za kupitia  rasimu ya mkataba, ili kuhakikisha zoezi hilo linafanyika kwa utaratibu rasmi na ulio wazi.

Amesema hatua hiyo ni utekelezaji wa maelekezo ya serikali yaliyolenga kuwapatia wafanyabiashara hao eneo mbadala baada ya kufungwa kwa soko lao la awali kufuatia maamuzi ya Mkuu wa Wilaya ya Dodoma.

Gondwe alieleza kuwa eneo la Umonga lililopo Mtaa wa Kitenge, Kata ya Majengo, lilipatikana baada ya kamati maalum iliyoundwa na Mkuu wa Wilaya kufanya tathmini ya maeneo mbalimbali kwa kushirikiana na viongozi wa wafanyabiashara na wataalam wa halmashauri, na kupendekeza eneo hilo kama suluhisho la kudumu.

Kwa mujibu wa Gondwe, Halmashauri tayari imeanza maandalizi ya msingi katika eneo hilo ikiwemo ujenzi wa vyoo na uwekaji wa kifusi katika maeneo yaliyokuwa na changamoto ya maji kutuama, ili kuweka mazingira rafiki kwa wafanyabiashara watakaoanza shughuli zao.

Alifafanua kuwa mpango wa uendelezaji wa eneo hilo unatekelezwa kwa awamu mbili, ambapo awamu ya kwanza inahusisha ujenzi wa vibanda vya muda vya mita 3x3 kwa gharama nafuu, huku awamu ya pili ikilenga ujenzi wa miundombinu ya kisasa kwa matumizi ya kudumu.

Aidha, Gondwe alibainisha kuwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Nchemba, alifanya ziara Februari, 2026 na kutembelea eneo hilo la Umonga, ambapo aliagiza kuharakishwa kwa mchakato huo pamoja na kuhakikisha wafanyabiashara wanapatiwa mikataba iliyo wazi na inayoeleweka kabla ya kuanza biashara.

Hata hivyo, amesema mchakato huo umekumbwa na changamoto baada ya baadhi ya wafanyabiashara kukataa kujadili rasimu ya mkataba na badala yake kuibua madai mapya ikiwemo kuongeza idadi ya wanufaika, kudai fidia ya miezi sita na kutaka kuanza biashara bila kukamilisha taratibu za mikataba.

Katika hatua nyingine, Mkuu wa Divisheni ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji wa halmashauri hiyo, Nsubi M. Kapula, amesema endapo viongozi wa wafanyabiashara hawatajitokeza kushiriki katika kupitia rasimu ya mkataba, halmashauri italazimika kuchukua hatua ya kukutana moja kwa moja na wafanyabiashara ili kuhakikisha shughuli zinaanza bila kuchelewa.

Amesema hadi sasa wameendelea kutoa wito kwa viongozi hao kushiriki mchakato huo, lakini endapo watakaidi, hawatasita kuchukua hatua mbadala kwa manufaa ya wafanyabiashara wote.

Kwa ujumla, halmashauri imesisitiza kuwa itaendelea kusimamia mchakato huo kwa kuzingatia sheria, taratibu na maelekezo ya serikali, huku ikiwataka wafanyabiashara kuepuka matapeli na kusubiri utaratibu rasmi wa ugawaji wa maeneo ili waweze kurejea katika shughuli zao bila migogoro.









Na Oscar Assenga, Tanga

Mkoa wa Tanga unaendelea kuandika historia mpya ya kiuchumi kufuatia kuongezeka kwa kasi kwa wawekezaji na kuimarika kwa miundombinu, hatua inayotajwa kuwa kichocheo kikubwa cha ukuaji wa biashara na mapato ya serikali.

Akifungua kikao cha Baraza la Biashara la Mkoa huo, Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Balozi Batilda Burian, alisema lengo la kikao hicho ni kujadili kwa kina namna ya kuboresha mazingira ya biashara ili yawe rafiki na wezeshi zaidi, pamoja na kuibua fursa za uwekezaji na kutafuta suluhisho la changamoto zinazoikabili sekta hiyo.

Alisema serikali inaendelea kuchukua hatua mbalimbali kuboresha mfumo wa kodi, akieleza kuwa tayari Rais aliunda tume maalum iliyopitia kodi mbalimbali na kutoa mapendekezo.

Alibainisha kuwa mkoa unasubiri utekelezaji wa mapendekezo hayo ili kusaidia kuondoa migongano ya kodi, hususan zile za halmashauri zilizokuwa zikilalamikiwa na wafanyabiashara.

Katika hatua nyingine, Balozi Burian alisema Tanga imekuwa kivutio kikubwa cha uwekezaji, huku Jiji la Tanga likiongoza kwa kupokea wawekezaji wengi zaidi.


Aliongeza kuwa uwekezaji huo sasa umeanza kusambaa hadi wilaya za Muheza na Korogwe, ambako kunatarajiwa kujengwa kiwanda kikubwa cha sukari pamoja na kuanzishwa kwa bandari kavu.

Akizungumzia mafanikio ya Bandari ya Tanga, alisema kumekuwa na ongezeko kubwa la shehena ya mizigo kutoka tani 470,000 sasa wanapokea zaidi ya tani milioni 1.3, jambo linalochochea ukuaji wa uchumi.

Alifafanua kuwa kwa sasa takriban meli 60 huingia bandarini kila mwezi, ikilinganishwa na meli 18 hapo awali, huku kila meli ikiingiza Bandarini wastani wa shilingi bilioni 2 kwa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).

“Tunafanya jitihada kuhakikisha ufanisi wa bandari unaongezeka zaidi kwa kupunguza muda wa kuhudumia meli na kuondoa msongamano, ili kuongeza tija kwa sekta binafsi na serikali kwa ujumla,” alisema.

Kuhusu miradi ya kimkakati, Balozi Burian alisema mradi wa bomba la mafuta wa EACOP umefikia hatua za mwisho, huku ukitarajiwa kuanza rasmi kupitisha mafuta kati ya mwezi Juni na Julai.

Alisema mradi huo tayari umetoa fidia ya zaidi ya shilingi bilioni 10 kwa wananchi na kutoa ajira kwa zaidi ya watu 1,700.

Katika sekta ya miundombinu, ujenzi wa barabara ya Tanga–Pangani unaendelea, licha ya changamoto za mvua, huku serikali ikiahidi kuhakikisha shughuli za biashara haziathiriki.

Aidha, uwanja wa ndege wa Tanga unaendelea kuboreshwa kwa gharama ya shilingi bilioni 63, ikiwa ni pamoja na ujenzi wa jengo la abiria, uzio na upanuzi wa njia ya kurukia ndege ili kuruhusu ndege kubwa kutua.

Kwa upande wa viwanda, serikali ya mkoa kwa kushirikiana na Wizara ya Viwanda na Biashara inaendelea kufuatlia viwanda vilivyokuwa vimekufa na kuvifufua viwanda vilivyokufa na kuvutia uwekezaji mpya.

Ikiwemo kutaka Maeneo ya uwekezaji yaliyotengwa kupitia TISEZA sasa yanasimamiwa kwa karibu zaidi na kuwekwa alama ili wawekezaji wanapokwenda waweze kuwekeza na tayari mwekezaji mmoja ameonyesha nia ya kujenga kiwanda cha nondo.

Sekta ya utalii nayo imeelezwa kuwa na fursa kubwa, hususan katika maeneo ya fukwe za Pangani na Mking ambapo alisema kwamba Pangani wana maeneo ya Kipumbwi wanayagawa kwa ajili ya uwekezaji kwenye fukwe na Mkinga katika maeneo ya Kwale na maeneo mengine ya Fukwe .


Aliongeza pia kwamba kuna uwekezaji mkubwa katika soko la Samaki na ni juzi tu Rais alizindua Meli kubwa ya Uvuvi wa Bahari ya Kuu na Meli hiyo itavua mpaka Tanga lakini katika meli nne zitakapotimia nadhani moja itakuja kufanya shughuli zake hapa Tanga .

Akisisitiza wana imani wataanza kutumia rasilimali za bahari kwa ufanisi na itakuwa na mchango mkubwa kutokana na kwamba kuwepo na masoko ya Samaki ikiwemo ,Mkinga,Tanga eneo la Deepsea na soko la Samaki la Kimataifa la Kipumbwi.

Sambamba na hilo, uwekezaji katika uvuvi wa bahari kuu unatarajiwa kuongeza upatikanaji wa samaki na kuimarisha masoko, ikiwemo soko la kimataifa la samaki la Kipumbwi.

Awali, Katibu Tawala wa Mkoa wa Tanga, Rashid Mchatta, alisema Baraza la Biashara ni jukwaa muhimu linaloleta pamoja sekta ya umma na binafsi kwa lengo la kujenga mazingira bora ya biashara, kuimarisha uaminifu na kuhakikisha sekta binafsi inakuwa endelevu.

Kamanda wa Polisi mkoa wa Morogoro ACP Endrew Kantimbo amesimamia zoezi la uundaji wa vikundi sita vya ulinzi shirikishi katika vijiji vya wakulima   na wafugaji vilivyopo Kata ya  Melela Wilaya ya Mvomero Mkoani Morogoro.

Hili limekuja  Kufuatia kwa  matukio mfululizo ya wizi wa mifugo katika eneo hilo ambapo wananchi hao wamesisitizwa kujilinda wenyewe kwa kushirikiana na Polisi kata wa eneo hilo.

Akizungumza na Wananchi hao  katika eneo la Melela Kituoni Mei 3, 2026 Kamanda Kantimbo amesema viongozi wa vijiji na wananchi kwa ujumla wanapaswa kushirikiana na vikundi hivyo katika kuzuia uhalifu pamoja na kuwatolea taarifa wahalifu ili wadhibitiwe mapema.

Kwa upande wake Mkuu wa Polisi wilaya ya Mvomero SSP Boniface Mwakalyegese amesema Wananchi watoe taarifa za uhalifu na kuacha kumaliza kesi kimila kwa kulipana Ng'ombe badala yake wafuate mnyororo wa sheria

Christopher Madukule  mfugaji kwa niaba ya wananchi wenzake amelishukuru Jeshi la Polisi Mkoa Morogoro kupitia Kamanda wake kwa kitendo cha  kutoka ofisini na katani kwaajili yao.

Naye, Sauda Kipira Mkulima wa eneo hilo amesema, mbali na kuzuia mifugo, Vikundi hivyo vinapaswa kuwadhibiti vijana wanaofanya matukuo ya ukatili wa kijinsia kwa watoto wakike pindi wanapotumwa.






Waziri wa Afya Mhe. Mohamed Mchengerwa amewataka viongozi na watumishi wa sekta ya afya kuzingatia kutoa huduma za staha, utu na huruma kwa wananchi na kufuata maadili ya kada zao

Waziri Mchengerwa ameyasema hayo leo Mei 3, 2026, jijini Mwanza wakati akifungua kikao kazi cha Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Wizara ya Afya

Amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuwekeza kwa kiwango kikubwa katika kuboresha miundombinu ya afya nchini, ikiwa ni pamoja na ununuzi wa mashine za kisasa kama MRI, CT-Scan na vifaa vya kusafisha figo pamoja na ukarabati wa vituo vya kutolea huduma.

“Uwepo wa majengo mazuri na vifaa vya kisasa hauwezi kuwa na maana endapo huduma zinazotolewa hazina utu na huruma kwa wagonjwa,” amesema Mhe. Mchengerwa

Mhe. Mchengerwa ameongeza kuwa lugha chafu, rushwa, upendeleo na uzembe vinaweza kufuta kabisa thamani ya uwekezaji mkubwa uliofanywa na Serikali katika kuboresha sekta hiyo muhimu.

Aidha, Mhe. Mchengerwa amewataka watumishi kuhakikisha huduma zinatolewa kwa weledi, heshima na uadilifu, huku akionya kuwa, vitendo vya kuchelewesha huduma bila sababu, kudhalilisha wagonjwa au kuomba rushwa havitavumiliwa.

“Mgonjwa anapofika Hospitalini mara nyingi hubeba maumivu na hofu, hivyo namna anavyopokelewa inaweza kuwa sehemu ya tiba au kuongeza mateso zaidi,” amesisitiza

Ameongeza kuwa “Viongozi ndani ya Wizara ya Afya niwakumbushe kuwa uongozi bora hauhusiani na vitisho au ubabe, bali ni uwezo wa kusimamia, kuelekeza na kusahihisha kwa staha na heshima, malalamiko ya matumizi mabaya ya madaraka, unyanyasaji na udhalilishaji wa Watumishi wa ngazi za chini hii ni changamoto inayopaswa kushughulikiwa kwa umakini na kwa mujibu wa sheria,”

Mwisho, Waziri Mchengerwa ameleeza kuwa Serikali itaendelea kuimarisha mifumo ya kusikiliza na kushughulikia malalamiko ili kuhakikisha Watumishi wote wanafanya kazi katika mazingira salama, yenye heshima na yanayolinda utu wao.





Dating siku hizi? Hapana… hiyo ni full-time job ambayo haina contract.

Unapambana na kazi mchana, usiku unapambana na feelings.

Mtu anakutumia “good morning babe” leo, kesho anakuacha kwenye blue ticks kama umetuma application ya kazi. No response. No update. Hakuna hata “seen with respect.”

Unajiuliza: shida iko wapi? Kadri unavyofikiria, ndivyo unachoka zaidi.
Ukweli ni huu—mahusiano mazuri si rahisi. Na consistency? Hiyo ni luxury.

Watu wanabadilika. Mood zinabadilika. Kitu pekee kinachobaki consistent ni confusion… na machozi ya kiwango cha juu kidogo.

Halafu kuna vitu vingine vidogo vinavyokuja kuku-save. Kama baridi ya jioni baada ya siku ndefu.

Kama funda la kwanza la kinywaji kilichotengenezwa vizuri kwa ustadi. Gordon’s Premix Cocktail waliinielewa kidogo hapo.

Unajua ile feeling ya kufungua kitu, na unajua kabisa kitakuwa sawa?
Hakuna masuala ya kukisia. Hakuna “leo itakuwaje?”
Gordon’s Premix ni perfectly mixed. Tamu. And always consistent.

Tofauti na baadhi ya watu—hii haina mixed signals. Baada ya siku ya emails zisizoisha na chats zisizojibiwa, unahitaji kitu ambacho hakikuchoshi kufikiria.


Hakuna “tonic imeisha.” Hakuna “subiri kidogo.” Hakuna drama.
Unachofungua, ndicho unachokipata.

Na labda hapo ndipo somo lilipo. Especially ikiwa baridi na mvua hizi zinazoendelea.

Consistency sio kelele. Sio promises nyingi.
Ni ile hali ya kujua—hata bila kuuliza—kila kitu kiko sawa.

Watu watafanya ugumu uwe mgumu zaidi.
Lakini angalau, si kila kitu maishani kinahitaji effort hiyo.

Vingine… vinafanya tu kazi.

Kama ile cocktail in a bottle, Gordon’s Premix.

@Gordon's_ea
#PerfectPair #YouMeAndGordonsTonic


Na Janeth Raphael- MichuziTv

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesisitiza kuwa uhusiano kati ya Tanzania na Rwanda hauishii kuwa wa ujirani tu, bali ni wa kindugu wa kihistoria uliodumu kwa miaka mingi hata kabla ya ukoloni. Amesema kufanana kwa mila, tamaduni na historia ni ushahidi wa undugu huo wa karibu unaowaunganisha wananchi wa mataifa haya mawili.

Akizungumza baada ya mazungumzo rasmi na Rais wa Rwanda, Paul Kagame, aliyefanya ziara ya siku moja nchini Tanzania, Rais Samia alieleza kuwa nchi hizi mbili zimeendelea kushirikiana kwa karibu katika ngazi za kikanda na kimataifa. Ushirikiano huo unajumuisha Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), Umoja wa Afrika (AU), pamoja na Umoja wa Mataifa (UN).

Katika nyanja ya uchumi, Rais Samia alibainisha kuwa biashara kati ya Tanzania na Rwanda imekua kwa kiwango kikubwa, ikifikia thamani ya shilingi bilioni 644 katika mwaka uliopita. Aidha, kuanzia mwaka 1997 hadi Machi mwaka huu, Tanzania imesajili miradi 42 ya uwekezaji kutoka Rwanda yenye thamani ya dola za Marekani milioni 325.5, ambayo imezalisha ajira kwa Watanzania 2,225.

Kwa lengo la kuongeza ukuaji wa uchumi, nchi hizo mbili zimekubaliana kuondoa vikwazo visivyo vya kikodi vinavyokwamisha biashara. Hatua hiyo inalenga kurahisisha matumizi ya soko la pamoja la Afrika Mashariki pamoja na soko huria la bara la Afrika.

Katika sekta ya nishati, Rais Samia alitaja mradi wa pamoja wa kuzalisha umeme katika maporomoko ya Rusumo unaoshirikisha Tanzania, Rwanda na Burundi. Mradi huo una uwezo wa kuzalisha megawati 80 za umeme, na mipango inaendelea kuuzindua rasmi.

Pia, makubaliano yamefikiwa kati ya Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na Shirika la Umeme Rwanda kuanza biashara ya kuuziana umeme, hatua inayotarajiwa kuongeza upatikanaji wa nishati na kuchochea maendeleo ya kiuchumi katika nchi hizo mbili.

Kwa ujumla, ziara hiyo imeimarisha zaidi uhusiano wa kidiplomasia na kiuchumi kati ya Tanzania na Rwanda, huku viongozi wakisisitiza kuendeleza ushirikiano kwa manufaa ya wananchi wao na kanda kwa ujumla.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiongoza Ujumbe wa Tanzania kwenye mazungumzo na Ujumbe wa Rwanda uliongozwa na Rais wa Nchi hiyo Mhe. Paul Kagame, tarehe 03 Mei, 2026.




Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Waandishi wa Habari kuhusu Ziara ya Kikazi ya Rais wa Jamhuri ya Rwanda Mhe. Paul Kagame, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 03 Mei, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Rwanda Mhe. Paul Kagame akizungumza na Waandishi wa Habari kufuatia Ziara yake ya Kikazi Jijini Dar es Salaam, tarehe 03 Mei, 2026


Matukio mbalimbali katika Ziara ya Kikazi ya Rais wa Jamhuri ya Rwanda Mhe. Paul Kagame, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 03 Mei, 2026.


Top News