Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Mboni Mhita akikata keki na kuzindua kikundi cha Wanawake Chuma katika Tamasha la Mwanamke Chuma Msimu wa Tano -Picha - Malunde


Na Kadama Malunde, Malunde 1 Blog


Mamía ya wanawake wamejitokeza kushiriki Tamasha la Mwanamke Chuma Msimu wa Tano lililofanyika Aprili 11, 2026 katika Ukumbi wa Malex uliopo Kahama, mkoani Shinyanga, huku wito ukitolewa kwa wanawake kushirikiana na kuinua wenzao ili kufikia mafanikio ya pamoja.


Mgeni rasmi katika tamasha hilo alikuwa Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Mboni Mhita, aliyesisitiza umuhimu wa mshikamano, uthubutu na kujiamini kwa wanawake katika harakati za maendeleo binafsi na ya jamii.


Akizungumza katika tamasha hilo, Mhita amewataka wanawake kuacha hofu ya maneno ya watu na badala yake kuzingatia malengo yao kwa vitendo.


“Mwanamke hakikisha unapambana ili kufikia malengo yako, usiogope kusemwa. Wewe songa mbele kwa sababu uwe mzuri utasemwa, uwe mbaya utasemwa, upendeze utasemwa, usipendeze utasemwa. Kuna watu wamevunjika moyo kwa sababu ya kusemwa, hakikisha kuwa upo na watu sahihi, jiamini, usihangaike na watu wenye kukutisha tamaa. Ili mwanamke uonekane umefanikiwa, lazima uinue wanawake wenzako. Uwe nguzo ya kuwainua wengine,” amesema Mhita.

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Mboni Mhita.


Akifafanua zaidi, Mhita amebainisha kuwa katika dunia ya sasa, mafanikio ya mwanamke yanategemea zaidi uthubutu wa kiuchumi, akisisitiza kuwa, “siri ya mwanamke yoyote ni sasampa (pesa), na habari ya mjini ni pesa, hivyo ni lazima mwanamke uhakikishe unazitafuta na kuzitumia fursa zinazokuwezesha kuinuka kiuchumi.”


Ameongeza kuwa wanawake wanapaswa kujiamini na kutumia kikamilifu fursa zilizowekwa na serikali, ikiwemo mikopo na uwezeshaji katika sekta mbalimbali kama madini, kilimo na viwanda, akibainisha kuwa mazingira rafiki yameboreshwa chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan.


Amesema kuwa kupitia maboresho hayo, wanawake wachimbaji wa madini sasa wanapata mikopo na kushiriki kikamilifu katika shughuli za uzalishaji, huku sekta ya kilimo ikipewa kipaumbele kwa kuongeza bajeti ili wanawake wanufaike zaidi.


Aidha, ameeleza kuwa hata katika sekta ya viwanda wanawake wameendelea kunufaika na fursa zilizopo na kuchangia ukuaji wa uchumi.

Mhita amewapongeza wanawake wa Ushetu kwa jitihada zao katika kusindika na kuongeza thamani ya mazao, akieleza kuwa huo ni mfano bora wa namna wanawake wanavyoweza kutumia fursa za kiuchumi kujiletea maendeleo endelevu.


Pia amegusia mafanikio yaliyopatikana katika sekta ya afya na elimu, akieleza kuwa Serikali imeendelea kuboresha huduma za afya kwa wananchi, huku Mkoa wa Shinyanga ukiwa sasa na shule sita za wasichana, hatua inayochochea upatikanaji wa elimu kwa mtoto wa kike na kumjengea msingi imara wa mafanikio ya baadaye.


Akisoma risala kwa mgeni rasmi, Mkurugenzi wa Gold FM na mwandaaji wa tamasha hilo, Bi. Neema Mghen, amesema Tamasha la Mwanamke Chuma limeendelea kuwa zaidi ya tukio la kawaida na sasa ni jukwaa muhimu la mabadiliko kwa wanawake.

Neema Mghen


Amesema kupitia tamasha hilo, wanawake wengi wamefanikiwa kujikwamua kiuchumi, kujitambua, kujiamini na kushiriki kikamilifu katika nafasi za uongozi na maamuzi ndani ya familia na jamii.


Kaulimbiu ya mwaka huu, “Nguvu ya Ujasiri,” imelenga kuhamasisha wanawake kusimama bila uoga, kuchukua hatua na kutumia fursa zilizopo kubadilisha maisha yao na ya wengine.


Ametaja mafanikio ya msimu wa tano kuwa ni pamoja na kuanzishwa kwa kikundi cha Mwanamke Chuma Maendeleo Group kilichozinduliwa rasmi wakati wa Tamasha la Mwanamke Chuma 2026, kusaidia wanawake wa gereza la Kahama kwa kuwapatia mahitaji muhimu, pamoja na kuendeleza utamaduni wa kutoa tuzo kwa wanawake ili kutambua na kuhamasisha juhudi zao.

Hata hivyo, amebainisha changamoto zinazowakabili wanawake kuwa ni pamoja na ukosefu wa mitaji na utaalamu katika sekta ya uchimbaji mdogo wa madini, uwepo wa mikopo yenye riba kubwa na masharti magumu, pamoja na changamoto za pembejeo bora na masoko ya uhakika katika sekta ya kilimo.


“Tunaamini ukimuinua mwanamke, umeinua familia na jamii kwa ujumla. Ujasiri wa mwanamke si kelele bali ni hatua, si maneno bali ni matendo,” amesema Mghen.


Ameongeza kuwa Tamasha la Mwanamke Chuma lina lengo la kukuza uchumi wa wanawake mmoja mmoja na vikundi, kujenga mshikamano, uthubutu na kuimarisha sauti ya pamoja ya wanawake katika maendeleo ya kijamii na kiuchumi.


Katika tamasha hilo lililoandaliwa na Kituo cha Redio cha Gold FM, viongozi mbalimbali wamehudhuria akiwemo Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga SACP Janeth Magomi, Mbunge wa Ushetu Mhe. Emmanuel Cherehani na Mbunge wa Kahama Mjini Mhe. Benjamini Ngayiwa, pamoja na wadau mbalimbali wa maendeleo.
Tamasha hilo limepambwa na burudani kutoka kwa msanii mkongwe wa muziki wa taarab, Mzee Yusuph, huku uendeshaji wa shughuli ukifanywa na MC maarufu Dkt. Kumbuka na mtaalamu wa maendeleo ya familia na uchumi, Dkt. Chris Mauki, aliyetoa mada mbalimbali zilizolenga kuwainua wanawake kiuchumi na kijamii.


Aidha, jumla ya tuzo tisa za ushindani zimetolewa kwa washindi waliopatikana kupitia kura za wananchi, pamoja na tuzo maalum za heshima na vyeti kwa wadau waliotoa mchango mkubwa katika kuwawezesha wanawake.


Tuzo hizo zimetolewa kwa wanawake waliobobea katika nyanja mbalimbali zikiwemo ujasiriamali, madini, ubunifu, ushonaji, upishi, saluni pamoja na wanawake wenye ushawishi chanya katika jamii, hatua inayolenga kuhamasisha wanawake wengine kujituma na kufikia mafanikio.


ANGALIA MATUKIO KATIKA PICHA

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Mboni Mhita akizungumza kwenye Tamasha la Mwanamke Chuma Msimu wa Tano lililofanyika Aprili 11, 2026 katika Ukumbi wa Malex uliopo Kahama, mkoani Shinyanga - Picha na Kadama Malunde - Malunde 1 blog


Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Mboni Mhita akizungumza kwenye Tamasha la Mwanamke Chuma Msimu wa Tano lililofanyika Aprili 11, 2026 katika Ukumbi wa Malex uliopo Kahama, mkoani Shinyanga

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Mboni Mhita akizungumza kwenye Tamasha la Mwanamke Chuma Msimu wa Tano lililofanyika Aprili 11, 2026

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Mboni Mhita akiimba na kucheza na Wanawake Chuma kwenye Tamasha la Mwanamke Chuma Msimu wa Tano

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Mboni Mhita akizindua kikundi cha Wanawake Chuma katika Tamasha la Mwanamke Chuma Msimu wa Tano

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Mboni Mhita akikabidhi katiba ya kikundi cha Wanawake Chuma katika Tamasha la Mwanamke Chuma Msimu wa Tano

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Mboni Mhita akikata keki katika Tamasha la Mwanamke Chuma Msimu wa Tano

Mwandaaji wa Tamasha la Mwanamke Chuma 2026 ambaye pia ni Mkurugenzi wa Kituo cha Redio cha Gold FM, Bi. Neema Mghen akisoma risala kuhusu Tamasha la Mwanamke Chuma

Mwandaaji wa Tamasha la Mwanamke Chuma 2026 ambaye pia ni Mkurugenzi wa Kituo cha Redio cha Gold FM, Bi. Neema Mghen akisoma risala kuhusu Tamasha la Mwanamke Chuma

Mbunge wa Jimbo la Ushetu Mhe. Emmanuel Cherehani akizungumza katika Tamasha la Mwanamke Chuma 2026

Mbunge wa Jimbo la Kahama Mjini Mhe. Benjamini Ngayiwa akizungumza katika Tamasha la Mwanamke Chuma 2026

Mwandaaji wa Tamasha la Mwanamke Chuma 2026 ambaye pia ni Mkurugenzi wa Kituo cha Redio cha Gold FM, Bi. Neema Mghen akikabidhi tuzo ya Heshima kwa Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mhe. Mboni Mhita. Kushoto ni Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga SACP Janeth Magomi

Mtaalamu wa maendeleo ya familia na uchumi, Dkt. Chris Mauki akitoa mada kwenye tamasha la Mwanamke Chuma 2026

Mtaalamu wa maendeleo ya familia na uchumi, Dkt. Chris Mauki akitoa mada kwenye tamasha la Mwanamke Chuma 2026





Msanii Mkongwe wa Taarabu, Mzee Yusuph akitoa Burudani

Msanii Mkongwe wa Taarabu, Mzee Yusuph akitoa Burudani










































TAZAMA PICHA ZAIDI HAPA - TAMASHA LA MWANAMKE CHUMA 2026


Meneja wa Mahusiano ya Jamii na Mazingira wa Mgodi wa Barrick Bulyanhulu , Bw Agapiti Paul (kushoto) akibadilishana mkataba wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo kupitia (CSR) Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Nyang’hwale, John Isack (kulia) wengine pichani ni maofisa waandamizi wa halmashauri hiyo.

Meneja wa Mahusiano ya Jamii na Mazingira wa Mgodi wa Barrick Bulyanhulu , Bw. Agapiti Paul akiongea katika hafla ya kusaini mkataba wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo kupitia (CSR) katika Halmashauri ya Wilaya ya Nyang’hwale.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Nyang’hwale, John Isack akiongea katika hafla ya kusaini mkataba wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo kupitia (CSR) katika Halmashauri ya Wilaya ya Nyang’hwale.

Meneja wa Mahusiano ya Jamii na Mazingira wa Mgodi wa Barrick Bulyanhulu , Bw Agapiti Paul akisaini mkataba.



#Mgodi kutoa shilingi milioni 900 kwa utekelezaji wa miradi ya mwaka huu


Uwekezaji wa kampuni ya Barrick nchini yenye ubia Serikali nchini kupitia kampuni ya Twiga unazidi kuleta manufaa kwa wananchi ambapo mgodi wa Barrick Bulyanhulu uliopo wilayani Msalala na Nyang’hwale umesaini mkataba na Halmashauri ya Wilaya ya Nyang’hwale ambapo katika kipindi cha mwaka huu utatoa kiasi cha shilingi milioni 900 za uwajibikaji kwa jamii (CSR) kwa ajili ya kufanikisha miradi mbalimbali ya maendeleo.


Hafla ya kusaini mkataba huo imefanyika katika ukumbi wa mikutano wa Halmashauri hiyo na kushuhudiwa na viongozi mbalimbali kutoka Ofisi ya Mkuu wa Wilaya, Ofisi ya Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri na Wafanyakazi wa Barrick Bulyanhulu.


Mwenyekiti wa Halmashauri ya Nyang’hwale, John Isack John, akiongea katika hafla hiyo amesema kuwa fedha hizo zitawezesha kutekelezwa kwa miradi mbalimbali 9 katika sekta mbalimbali ikiwemo elimu, afya, fedha, utawala,maendeleo ya jamii, mali asili na uhifadhi wa mazingira.


Ameitaja miradi itakayotekelezwa kuwa ni ujenzi wa soko la dhahabu (awamu ya kwanza),ufugaji wa nyuki katika msitu wa Miyenze,ujenzi wa nyumba ya mtumishi na uchimbaji wa kisima katika shule ya sekondari Iyenze pamoja na ununuzi wa vitanda 240 kwa mabweni ya shule za sekodari za Bukwimba, Busolwa na Kenegele.


Aidha, miradi mingine ni pamoja na ununuzi wa madawati na samani za walimu katika Shule Mpya ya Msingi Sengerema, ukamilishaji wa miundombinu ya maji na umeme katika Zahanati ya Mwabui, ununuzi wa vifaa vya TEHAMA kwa watendaji wa vijiji na kata ya Mwingiro, pamoja na uchimbaji wa rambo la kunyweshea mifugo katika kijiji cha Ng’wasabuka.


Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Nyang’hwale, John Isack amesema ni muhimu miradi yote iliyopangwa kutekelezwa ikamilike kwa wakati ili iweze kuleta matokeo chanya kwa jamii husika.


“Tunataka miradi hii hasa ya elimu kama ni madawati , vitanda , ujenzi wa mabweni na nyumba za watumishi katika sekta ya elimu zikamilike kwa wakati na muda uliopagwa,” amesema Isack.


Ametoa wito kwa madiwani na Watalamu wa Halmashauri hiyo kuwatangazia wananchi miradi hii inayotekelezwa na fedha za uwajibikaji kwa Jamii (CSR) kutoka mgodi wa Barrick Bulyanhulu, ili wafahamu umuhimu wa kuwepo mgodi huu katika eneo lao.


Kuhusiana na ufanisi wa miradi inayotekelezwa na fedha za CSR kutoka Barrick Bulyanhulu, Isack amesema ufanisi wa utekelezaji wa miradi ya CSR katika wilaya hiyo umekuwa ukizidi kuwa bora mwaka hadi mwaka na kwa sehemu kubwa utajikita kwenye miradi ya kijamii ambayo ni vipaumbele vya wananchi wa maeneo husika.


Kwa upande wake Mwakilishi wa Barrick katika hafla hiyo ambaye ni Meneja wa Mahusiano ya Jamii na Mazingira wa Mgodi wa Barrick Bulyanhulu , Bw. Agapiti Paul amesema fedha hizo za CSR zitatatumika kufanikisha miradi ya maendeleo kama vile elimu , afya , uboreshaji wa miundombinu na ujenzi wa nyumba za watumishi katika sekta ya elimu na afya.


“Kwa kweli mwaka huu katika miradi iliyonipa furaha na ujenzi wa soko la dhahabu hapa Nyang’hwale ambapo itakuwa ni chanzo kikuu cha uchumi na itaongeza thamani ya miradi ya kijamii na kuwa chanzo cha ukuaji wa uchumi kwa wachimbaji wadogo na vile vile ni kichocheo cha kusukuma miradi mengine ya maendeleo kama vile elimu , afya , barabara na shughuli zingine za uzalishaji mali”, amesema Paul.


Amefafanua kwamba katika kuhakikisha wananchi wananufaika na uchimbaji madini, Mgodi wa Barrick utaendelea kuisaidia jamii zinazozunguka mgodi huo kwa kutekeleza miradi mbalimbali ikiwemo ujenzi wa shule, hospitali na barabara.


Katika kipindi cha mwaka uliopita mgodi wa Barrick Bulyanhulu ulitoa kiasi cha shilingi bilioni 1 na milioni 75 za uwajibikaji kwa jamii (CSR) ambazo zimefanikisha miradi miradi mbalimbali ya kijamii ya kuboresha maisha ya wananchi.



Meneja wa Mahusiano ya Jamii na Mazingira wa Mgodi wa Barrick Bulyanhulu , Bw. Agapiti Paul akiongea katika hafla ya kusaini mkataba wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo kupitia (CSR) katika Halmashauri ya Wilaya ya Nyang’hwale.

Meneja wa Mahusiano ya Jamii na Mazingira wa Mgodi wa Barrick Bulyanhulu , Bw. Agapiti Paul akiongea katika hafla ya kusaini mkataba wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo kupitia (CSR) katika Halmashauri ya Wilaya ya Nyang’hwale.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Nyang’hwale, John Isack akiongea katika hafla ya kusaini mkataba wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo kupitia (CSR) katika Halmashauri ya Wilaya ya Nyang’hwale.

















Top News