Na. Josephine Majura, WF, Dodoma
SERIKALI kupitia Wizara ya Fedha imeendelea kutekeleza mikakati ya kuimarisha uchumi wa wananchi kwa kuwezesha upatikanaji wa mitaji kupitia mikopo yenye masharti nafuu ili kuongeza uwezo wa kukopesheka kwa wafanyabiashara wadogo na wa kati, sambamba na kukuza miradi ya kiuchumi inayochangia pato la Taifa.

Hayo yameelezwa bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Deogratius Luswetula (Mb), alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Msalala, Mhe. Mabula Johnson Magangila, aliyetaka kujua lini Serikali itaanza kutumia rasilimali zake kama dhamana ili wafanyabiashara wa Kitanzania waweze kukopesheka zaidi.

Mhe. Luswetula, alisema Serikali imeweka utaratibu wa kutumia rasilimali zake kama dhamana, ambapo kupitia Benki ya NMB, wafanyabiashara wadogo na wa kati wanapatiwa mikopo kwa riba nafuu ya asilimia 7 kwa mwaka.

“Mpango huu unalenga kupunguza changamoto za kifedha zinazowakabili wajasiriamali na kuongeza ajira kwa wananchi “, alifafanua Mhe. Luswetula.

Aidha, alisema kuwa Serikali imeipatia Benki Kuu ya Tanzania jukumu la kusimamia Mifuko ya Udhamini wa Mikopo, ambayo inatoa udhamini kwa Watanzania wenye miradi yenye tija lakini wanaokabiliwa na changamoto za dhamana wakati wa kuomba mikopo.

Mhe. Luswetula, aliongeza kuwa kupitia mfumo huo, wananchi wanapata nafasi ya kufanikisha miradi yao bila kuzuiwa na vikwazo vya dhamana.

Kwa upande wa Wafanyabiashara wanaojihusisha na mauzo nje ya nchi, Mhe. Luswetula, alisema Serikali imeanzisha Mfuko wa Udhamini wa Mikopo ya Mauzo Nje ya Nchi (Export Credit Guarantee Scheme), huku wajasiriamali wadogo na wa kati wakinufaika kupitia Mfuko wa Udhamini wa Mikopo kwa Wajasiriamali Wadogo na wa Kati (SMEs Credit Guarantee Scheme).

Alisema kuwa juhudi hizo zote zinazofanywa na Serikali zina lengo la kurahisisha upatikanaji wa mikopo, kukuza miradi ya kiuchumi, na kuongeza tija katika sekta zote za uchumi.

Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Deogratius Luswetula (Mb), akijibu swali la Mbunge wa Msalala, Mhe. Mabula Johnson Magangila, aliyetaka kujua wakati ambao Serikali itaanza kutumia rasilimali zake kama dhamana ili wafanyabiashara wa Kitanzania waweze kukopesheka zaidi.
(Picha na Kitengo cha Mawasilino Serikalini, Wizara ya Fedha, Dodoma)




KUFUATIA uzushi na uvumi wa baadhi ya watu kuzua taharuki na kueleza kuibiwa nyeti zao baada ya kuguswa bega hali iliyopelekea vitendo vya uvunjifu wa amani ikiwemo vurugu na kusababisha baadhi ya watu kushambuliwa, kujeruhiwa na wengine kupoteza mali zao.


Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya lilifanya misako dhidi ya watu hao na kufanikiwa kuwakamata watuhumiwa 85 kwa tuhuma hizo, kati ya watuhumiwa 16 wameshafikishwa mahakamani, watuhumiwa 69 taratibu za kisheria zinakamilishwa ili waweze kufikishwa mahakamani.

Aidha, Aprili 09, 2026 watuhumiwa watatu ambao ni Onia Bahati Sanga [20] mkazi wa Ntokela na Regan Joshua Kaseke [20] mkazi wa Uyole walifikishwa Mahakama ya Mwanzo Wilaya ya Rungwe. Watuhumiwa walitenda kosa hilo kati ya Aprili 5 na 6, 2026 huko Ntokela, Wilaya ya Rungwe.

Mtuhumiwa Hashimu William Mwanasenga [29] mkazi wa Mahango alifikishwa Mahakama ya Mwanzo Ilongo Wilaya ya Mbarali baada ya Kutenda kosa hilo Aprili 7, 2026 katika Kijiji cha Mahango Wilaya ya Mbarali.

Watuhumiwa wote watatu walitiwa hatiani na kuhukumiwa kifungo cha miezi sita jela kila mmoja kwa kosa la kutoa taarifa za uongo na kuzua taharuki kwa kueleza kuibiwa nyeti zao baada ya kushikwa bega.

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya linatoa wito kwa baadhi ya watu wanaozua taharuki na kutoa taarifa za uzushi zinazosababisha vitendo vya uvunjifu wa amani kuacha mara moja. Aidha, Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya linakemea na kutoa onyo kali kwa wale wanao andaa maudhui ya uongo na kusambaza kwenye mitandao ya kijamii kuacha kwani hatua kali za kisheria zitaendelea kuchukuliwa dhidi yao.

Imetolewa na:
Kamanda wa Polisi,
Mkoa wa Mbeya.
Na Mwandishi Wetu


MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Tanzania Bara Stephen Wasira amesema mawazo ya Hayati Mwalimu Julius Nyerere akiwa Chuo Kikuu cha Makerere nchini Uganda aliandika kitabu cha kutetea wanawake ingawa kitabu hicho hakijachapishwa hadi amefariki.

Wasira ameyasema hayo leo Aprili 10, 2026 katika kongamano la kumbukizi ya Hayati Mwalimu Julius Nyerere, lililofanyika Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere, Kigamboni Dar es Salaam.

Amesema Mwalimu Nyerere aliandika kitabu cha ‘Uhuru wa Wanawake’ ambacho kilijikita kutetea usawa wa kijinsia, hata hivyo hadi anafariki dunia kilikuwa hakijachapishwa.

Akitoa ufafanuzi huo, amesema sababu ya Mwalimu Nyerere kuandika kitabu hicho ni kutetea wanawake waliokuwa wakiishi familia za Kiafrika zilizoathiriwa na ukosefu wa usawa wa kijinsia.

““Mwalim Nyerere thinking yake ilikuwa ni watu na katika mambo aliyofanya akiwa Makerere ni kuandika kitabu ambacho hakikuchapishwa hadi amefariki kinazungumzia uhuru wa wanawake ambacho kinaitwa Women are not chicken they Egle

“Wanawake wa Tanzania ni mashahidi katika hili kwani, Hayati Mwalimu Nyerere ndani ya kitabu hicho aliibua masuala muhimu na kusisitiza umuhimu wa ushiriki wa wakawake katika uongozi, utawala na maendeleo ya taifa kwa ujumla,” amesema.

Amebainisha kuwa, falsafa kuu ya uongozi wa Mwalimu Nyerere ilijikita katika misingi ya kulinda uhuru wa nchi, kuimarisha umoja wa taifa, kuleta maendeleo ya wananchi na kuendeleza harakati za ukombozi wa Afrika.











 

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Dkt. Fabian Madele, akihutubia wadau mbalimbali wa Sekta ya Mifugo, wakati wa warsha ya utambulisho wa Mradi wa Jenga Kesho Iliyo Bora (BBT) ya Unenepeshaji wa Mbuzi na Kondoo, uliyofanyika katika Ukumbi wa Chuo cha Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) - Kongwa, Aprili 9, 2026 Dodoma.

Mtaalam wa Ufuatiliaji na Tathmini wa Mradi wa Jenga Kesho Iliyo Bora (BBT) ya Unenepeshaji wa Mbuzi na Kondoo, ambaye ni Mchumi Mwandamizi Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI), Bw. Tumsime Mutta (aliyesimama), akielezea Mpango Mkakati wa Mradi, wakati wa warsha ya utambulisho wa Mradi huo, uliyofanyika katika Ukumbi wa Chuo cha Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) - Kongwa, Aprili 9, 2026 Dodoma.

Mtaalam wa Ufuatiliaji na Tathmini wa Mradi wa Jenga Kesho Iliyo Bora (BBT) ya Unenepeshaji wa Mbuzi na Kondoo, ambaye ni Mchumi Mwandamizi Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI), Bw. Tumsime Mutta (aliyesimama), akielezea Mpango Mkakati wa Mradi, wakati wa warsha ya utambulisho wa Mradi huo, uliyofanyika katika Ukumbi wa Chuo cha Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) - Kongwa, Aprili 9, 2026 Dodoma.

Mchungaji wa kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Ndg. Jeremia Nyato (aliyesimama), akitoa Ushauri wa namna ya kuwashawishi vijana kukimbilia fursa za unenepeshaji Mifugo, wakati wa warsha ya utambulisho wa Mradi wa Jenga Kesho Iliyo Bora (BBT) ya Unenepeshaji wa Mbuzi na Kondoo, uliyofanyika katika Ukumbi wa Chuo cha Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) - Kongwa, Aprili 9, 2026 Dodoma.

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Dkt. Fabian Madele (katikati), akijibu hoja mbalimbali za wadau wa Sekta ya Mifugo, wakati wa warsha ya utambulisho wa Mradi wa Jenga Kesho Iliyo Bora (BBT) ya Unenepeshaji wa Mbuzi na Kondoo, uliyofanyika katika Ukumbi wa Chuo cha Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) - Kongwa, Aprili 9, 2026 Dodoma, kulia ni Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Kongwa ambaye ni Afisa Tarafa ya Kongwa, Bw. Jerimia.

Picha ni baadhi ya wadau wa Sekta ya Mifugo wakimsikiliza Mgeni Rasmi ambaye ni Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Dkt. Fabian Madele (hayupo pichani), wakati wa warsha ya utambulisho wa Mradi wa Jenga Kesho Iliyo Bora (BBT) ya Unenepeshaji wa Mbuzi na Kondoo, uliyofanyika katika Ukumbi wa Chuo cha Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) - Kongwa, Aprili 9, 2026 Dodoma.

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Dkt. Fabian Madele (aliyekaa katikati), akiwa kwenye picha ya pamoja na wadau wa Sekta ya Mifugo, wakati wa warsha ya utambulisho wa Mradi wa Jenga Kesho Iliyo Bora (BBT) ya Unenepeshaji wa Mbuzi na Kondoo, uliyofanyika katika Ukumbi wa Chuo cha Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) - Kongwa, Aprili 9, 2026 Dodoma.

....

Wizara ya Mifugo na Uvuvi inayotekeleza Mradi wa miaka mitano wa Jenga Kesho Iliyo Bora (BBT) ya Unenepeshaji wa Mbuzi na Kondoo katika eneo la Kituo cha Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI) iliyopo Wilayani Kongwa, imepanga kuwawezesha vijana 200 wa Kitanzania kupata Mafunzo hayo ikiwa na lengo la kuongeza ushiriki wa vijana na wanawake katika ujasiliamali wa Biashara ya Mifugo.

Akizungumza leo Aprili 9, 2026 Wilayani Kongwa Jijini Dodoma kwa Niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, wakati wa warsha ya utambulisho wa Mradi huo, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Dkt. Fabian Madele, amesema mradi huo wenye thamani ya takribani shilingi Billioni 81, unalenga kuwawezesha vijana kupitia shughuli za unenepeshaji wa mbuzi na kondoo kibiashara, uzalishaji wa malisho na mbegu za malisho, uchakataji wa vyakula vya mifugo, pamoja na matumizi ya teknolojia za kisasa.

"Walengwa wakuu wa mradi huu ni vijana, ambao kupitia utekelezaji wake watapata ujuzi na uzoefu wa vitendo katika mnyororo mzima wa thamani wa mazao ya mifugo, hususan mbuzi, na kupitia mafunzo haya, vijana wetu watajengewa uwezo wa kuingia kwenye biashara za kisasa za mifugo na hivyo kujiongezea kipato pamoja na kuchangia ukuaji wa uchumi wa taifa." Amesema Dkt. Madele

Aidha, Dkt. Madele amesema baada ya vijana kupata ujuzi huo, matarajio ya Serikali ni kuwa vijana wataweza kujiajiri wenyewe, kuanzisha biashara zao, na kuwa sehemu ya suluhisho la changamoto ya ajira nchini, ambapo vijana watakaonufaika watakuwa na fursa ya kupatiwa mikopo isiyo na dhamana kwa ajili ya kuendeleza biashara zao baada ya mafunzo.

Vilevile, Dkt. Madele amebainisha kuwa matokeo ya kuwepo kwa Mradi huo ni kutokana na uongozi madhubuti wa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi mahiri wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kutambua kwa kina changamoto ya ukosefu wa ajira miongoni mwa vijana, ndiyo maana Mheshimiwa Rais amechukua juhudi za makusudi kuhakikisha fedha hizo zinapatikana kwa ajili ya kuboresha maisha ya vijana kupitia miradi yenye tija kama huo wa BBT.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Ufuatiliaji na Tathmini Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Ndg. Daudi Mayeji, amesema Mradi huo hautaishia kwa vijana waliopo Dodoma tu bali kwa vijana kutoka maeneo mbalimbali ya nchi, ambapo Mpango huo utamuwezesha kijana kuhudumia Mbuzi 100 kwa pamoja.

Pia, Ndg. Mayeji amesema Mradi huo unategemea ndani ya miaka mitano kutoa Mafunzo kwa vijana takriban 1750 na Serikali tayari imeshatenga eneo la hekta 2000 kwa ajili ya kupanda Malisho ya Mifugo.

Naye, Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Kongwa, ambaye ni Afisa Tarafa ya Kongwa, Ndg. Jeremiah Kabebwa ameishukuru Wizara kwa kuwaletea Mradi wenye fursa kwa vijana ambapo ameihakikishia Wizara kuwa Ofisi ya Mkuu wa Wilaya itahakikisha vijana wote wanaichangamkia fursa hiyo ili kuweza kujikwamua kiuchumi.

Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, ametoa maagizo kwa Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais – Maendeleo ya Vijana kuhakikisha vijana wa Kitanzania wananufaika kikamilifu na fursa zinazotokana na ukuaji wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA).

Akizungumza leo Aprili 10, 2026, Jijini Dodoma mara baada ya kuzindua minara 758 ya mawasiliano pamoja na kuimarishwa kwa mkongo wa taifa katika wilaya 85, Rais Samia alisema hatua hiyo ni muhimu katika kuchochea ajira na ubunifu kwa vijana.

Alisisitiza kuwa miundombinu hiyo inapaswa kutumika kikamilifu kuwawezesha vijana kujenga ujuzi wa kidijitali na kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi.

“Ni muhimu kuhakikisha vijana wetu wanapata fursa za kunufaika na uchumi wa kidijitali kupitia ubunifu, ajira na matumizi sahihi ya teknolojia,” alisema Rais Samia.

Aidha, Rais alielekeza kuwepo kwa mazingira rafiki kwa kampuni changa (start-ups) zinazomilikiwa na vijana, ikiwemo upatikanaji wa mitaji ili ziweze kukua na kushindana katika soko la ajira na biashara.

Katika kuimarisha juhudi hizo, aliwataka wadau wa sekta binafsi kushirikiana na serikali katika kukuza uwekezaji na ubunifu kwenye sekta ya TEHAMA, akibainisha kuwa vijana ndio nguvu kazi kuu ya uchumi wa kisasa unaotegemea maarifa na teknolojia.

Sambamba na hilo, Rais Samia alisisitiza umuhimu wa kulinda miundombinu ya mkongo wa taifa ili kuhakikisha inaendelea kutoa huduma bora na kuchangia maendeleo ya taifa.

Aidha Rais amesisitiza kuwa utekelezaji wa maagizo hayo utahakikisha hakuna kijana anayebaki nyuma katika safari ya kuelekea uchumi wa kidijitali jumuishi nchini.








Na, Mwandishi Wetu

Ujumbe wa Serikali ya Tanzania ukiongozwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Mhe. Profesa Palamagamba Kabudi, imekutana na Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola na Rais wa zamani wa Malawi, Mhe. Dkt. Lazarus McCarthy Chakwera, na kujadiliana kuhusu namna Tanzania ilivyojidhatiti katika kudumisha umoja, amani na mshikamano miongoni mwa Watanzania.

Kikao hicho kilifanyika katika Kituo cha Mikutano cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) siku ya Alhamisi Aprili 9, 2026 mchana baada ya Mheshimiwa Chakwera kumtembelea Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahamoud Thabit Kombo, ikiwa ni ishara ya kuanza rasmi kwa ziara ya Mjumbe huyo Maalum nchini Tanzania.

Katika kikao hicho, Mhe. Profesa Kabudi alimueleza kwa kina Mjumbe huyo Maalum, kuhusu hatua mbalimbali zinazoendelea kuchululiwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa lengo la kuimarisha demokrasia nchini huku ikiweka msisitizo katika kulinda na kuheshimu utu wa Mtanzania, kuzingatia haki na uwajibikaji, amani na utulivu pamoja na kudumisha umoja wa kitaifa.

“Tumekutana na Mheshimiwa Chakwera na tumemueleza mambo mengi kuhusu Tanzania na historia ya nchi hii tangu ipate uhuru mwaka 1961, hali ya siasa na demokrasia nchni, na hatua ambazo serikali inaendelea kuchukua ili kuhakikisha nchi inaendelea kuwa tulivu na kuwawezesha Watanzania kushiriki kikamilifu katika kujenga uchumi jumuishi na kujiletea maendeleo”, ameeleza Waziri Kabudi.

Waziri kabudi ameeleza kuwa kikao hicho kimekuwa kizuri na chenye mafanikio kutokana na Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola kupata ufafanuzi wa kutosha juu ya masuala mbalimbali yanayoendelea nchini hususani katika kudumisha amani, umoja wa kitaifa na ustawi wa Watanzania.

Mbali na kukutana na ujumbe wa Serikali, Mheshimiwa Chakwera anatarajiwa kukutana na wadau mbalimbali ambapo jana Aprili 10, 2026 alikutana na Msajili wa Vyama vya Siasa, Mhe. Jaji Mstaafu Francis Mutungi pamoja na vyama vya siasa vya ACT–Wazalendo, Chama cha National League for Democracy (NLD), United Democratic Party (UDP), Chama cha National Reconstruction Alliance (NRA), Chama cha NCCR Mageuzi, Chama cha Sauti ya Umma (SAU), Chama cha Alliance for Democratic Change (ADC), Alliance for African Farmers Party (AAFP) na Chama cha ADA-TADEA.

Vyama vingine ni pamoja na Democratic Party (DP), Tanzania Labour Party (TLP), Union for Multiparty Democracy (UMD), United People’s Democratic Party (UPDP), Chama cha Kijamii (CCK), Demokrasia Makini, Chama cha Ukombozi wa Umma (CHAUMA) na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA).

Katika ziara yake hii, Mheshimiwa Chakwera anatarajia pia kukutana na Mwenyekiti wa Tume ya Uchunguzi wa matukio yaliyotokea Oktoba 29, 2025 na baada ya Uchaguzi Mkuu, Jaji Mkuu Mstaafu Mhe. Mohamed Othman Chande, Waziri Mkuu Mstaafu na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jaji Joseph Warioba, Jumuiya zisizo za Kiserikali, Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar, Mhe. Jaji George Joseph Kazi, Mwenyekiti wa ACT – Wazalendo Mhe. Othman Masoud Othman, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Mussa Azzan Zungu, Jaji Mkuu wa Mahakama ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Jaji George Mcheche Masaju, Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufaa Mhe. Jacobs Mwambegele na Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi Mhe. Balozi Dkt. Asha-Rose Migiro.

Aidha, Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola, atakutana pia na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Hussein Ali Mwinyi, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi pamoja na Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.




 


Na Kadama Malunde - Kahama

Katika kuendeleza jitihada za kijamii na kuonesha mshikamano wa dhati kwa wanawake wenzao, Kikundi cha wanawake maarufu kinachojulikana kama Mwanamke Chuma Maendeleo Group kimetoa msaada wa vifaa mbalimbali kwa wafungwa wanawake katika Gereza la Kahama Mkoani Shinyanga, ikiwa ni sehemu ya maandalizi kuelekea kilele cha Tamasha la Mwanamke Chuma 2026 litakalofanyika Aprili 11, 2026 Mjini Kahama.


Msaada huo uliokabidhiwa unajumuisha mahitaji muhimu ya kila siku kama vile sabuni, taulo za kike, dawa za meno, nguo, lishe ya watoto, kandambili (ndala) pamoja na mafuta ya kujipaka ikiwa ni hatua ya kupunguza changamoto ndogondogo zinazowakabili wafungwa hao na wakati huo huo kuwapa faraja ya kihisia.


Akizungumza wakati wa kukabidhi msaada huo leo Ijumaa Aprili 10,2026 , Mwenyekiti wa Mwanamke Chuma Maendeleo Group, Bi. Neema Moshi, amesema kuwa hatua hiyo inatokana na dhamira ya kundi hilo kuhakikisha kuwa wanawake wote, bila kujali walipo, wanapata faraja na kuendelea kuamini katika thamani yao.

Neema Moshi akizungumza


“Tukiwa na kaulimbiu ya ‘Nguvu ya Ujasiri’, tumeona ni muhimu kuwafikia wanawake wenzetu waliopo gerezani ili kuwatia moyo na kuwaonesha kuwa hawako peke yao. Tumekuja kama wawakilishi wa wanachama wetu kuwapa ujumbe wa matumaini na mshikamano,” amesema Bi. Moshi.


Kwa upande wake, Mwandaaji wa Tamasha la Mwanamke Chuma 2026 ambaye pia ni Mkurugenzi wa Kituo cha Redio cha Gold FM, Bi. Neema Mghen, amesisitiza kuwa lengo kuu la ziara hiyo ni kuhamasisha matumaini na ujasiri kwa wanawake waliopo gerezani.

Neema Mghen akizungumza


“Tumekuja kuwaambia kuwa walipo si mwisho wa maisha yao. Ndoto zao bado zina thamani na wana nafasi ya kuanza upya. Wanapaswa kuendelea kuwa na ujasiri na kujiandaa kuwa wanawake imara watakapotoka hapa,” ameeleza Bi. Mghen.


Naye Mkuu wa Gereza la Kahama, Mrakibu Mwandamizi wa Magereza Bonis Njoka Gervas, ametoa shukrani kwa kundi hilo kwa msaada na faraja walioutoa, akieleza kuwa hatua hiyo inachangia kwa kiasi kikubwa katika mchakato wa urekebishaji wa wafungwa.

Bonis Njoka Gervas akizungumza


“Wafungwa wanahitaji sana faraja na kutiwa moyo. Msaada kama huu unasaidia kuleta utulivu na amani gerezani huku ukiwajengea matumaini wanapokuwa wakisubiri kumaliza vifungo vyao au kesi zao,” amesema.


TAMASHA LA MWANAMKE CHUMA 2026


Maandalizi ya Tamasha la Mwanamke Chuma 2026 yamekamilika, ambapo tukio hilo kubwa linatarajiwa kufanyika Jumamosi, Aprili 11, 2026 katika Ukumbi wa Malex Hall, Kahama kuanzia saa 11 jioni.


Tamasha hilo, linaloandaliwa na Kituo cha Redio cha Gold FM, limejipambanua kama jukwaa muhimu la kuwawezesha wanawake kijamii na kiuchumi kupitia elimu, mitandao na fursa mbalimbali.

Tamasha la mwaka huu linatarajiwa kupambwa na burudani mbalimbali kutoka kwa wasanii mbalimbali akiwemo msanii mkongwe wa muziki wa Taarab, Mzee Yusuph, huku mtaalamu wa maendeleo ya familia na uchumi, Dkt. Chris Mauki, akitoa mada maalum zitakazolenga kuwainua wanawake na jamii kwa ujumla.


Aidha, shughuli hiyo itasindikizwa na ucheshi na uchangamshi kutoka kwa MC maarufu, Dkt. Kumbuka.


Mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Mboni Mhita, ambaye atahitimisha rasmi tamasha hilo linalotarajiwa kuvuta washiriki kutoka maeneo mbalimbali ya Kanda ya Ziwa.


Mbali na burudani na elimu, tamasha hilo pia litahusisha utoaji wa tuzo kwa wanawake waliofanya vizuri katika nyanja mbalimbali, ikiwemo ubunifu, ujasiriamali, ushonaji, upishi, saluni pamoja na wanawake wenye ushawishi chanya katika jamii.


Kwa mujibu wa waandaaji, tamasha hilo ni zaidi ya burudani, ni jukwaa la kuibua vipaji, kuhamasisha uthubutu na kuimarisha mchango wa mwanamke katika maendeleo ya kijamii na kiuchumi.


Wananchi wa Kahama na maeneo jirani wanahimizwa kujitokeza kwa wingi kushiriki tukio hilo muhimu ambalo linabeba ujumbe wa matumaini, uthubutu na nguvu ya mwanamke wa kisasa.








Na Mwandishi wetu.

SERIKALI imepongeza hatua ya Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT) kwa kupata cheti cha viwango vya kimataifa cha ISO 21001:2018 kinachohusu mifumo ya usimamizi wa taasisi za elimu, hatua inayotarajiwa kuimarisha ubora wa mafunzo ya ufundi na teknolojia nchini.

Akizungumza jijini Dar es Salaam leo Aprili 10, 2026 kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Naibu Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Hussein Mohamed, amesema mafanikio hayo yanadhihirisha utekelezaji wa maono ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, ya kuimarisha elimu yenye ujuzi, ubunifu na tija kwa maendeleo ya uchumi wa taifa.

Amesema Serikali imeendelea kufanya uwekezaji mkubwa katika sekta ya elimu ili kuhakikisha vijana wanapata ujuzi unaoendana na mahitaji ya soko la ajira na viwanda.

“Mheshimiwa Rais amekuwa akisisitiza kuwa hatuhitaji elimu ya vyeti pekee, bali elimu yenye ujuzi, ubunifu na tija. Kupitia uwekezaji huu mkubwa, vijana wetu wataweza kujiajiri na kushiriki kikamilifu katika kujenga uchumi wa taifa,” amesema.

Naibu Katibu Mkuu huyo ameongeza kuwa mafanikio ya DIT yanaonesha umuhimu wa kuunganisha elimu na sekta ya viwanda ili wahitimu waweze kuwa sehemu ya uzalishaji na maendeleo ya uchumi unaotegemea sayansi na teknolojia.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Viwango Tanzania Tanzania Bureau of Standards (TBS), Ashura Katunzi, amesema utoaji wa cheti hicho unaonesha kuwa taasisi hiyo imekidhi viwango vya kimataifa katika utoaji wa huduma za elimu.

Amesema DIT imekuwa taasisi ya kwanza nchini kupata cheti hicho cha ISO 21001:2018, hatua inayothibitisha kuwa mfumo wake wa usimamizi wa elimu unazingatia ubora unaotambulika kimataifa.

“Cheti hiki ni ushahidi wa kazi kubwa, nidhamu na dira ya maendeleo ya taasisi. Kinaonesha kuwa wanafunzi wanaopata elimu hapa wanapewa maarifa yanayowaandaa kwa ajira na ushindani katika soko la dunia,” amesema Katunzi.

Naye Mwenyekiti wa Baraza la Taasisi hiyo, Masika, amesema hatua ya kupata cheti hicho ni matokeo ya safari ndefu ya maboresho ya mifumo ya uendeshaji iliyoanza mwaka wa fedha 2021/22, kwa lengo la kuhakikisha ubora wa elimu unatambulika kimataifa.

Ameeleza kuwa cheti hicho kinahusu kampasi zote tatu za taasisi hiyo ambazo ni Dar es Salaam, Mwanza na Songwe, na kwamba utekelezaji wake utaimarisha zaidi ubora wa mafunzo, kuongeza uaminifu kwa wanafunzi na wadau, pamoja na kuongeza ushindani wa wahitimu katika soko la ajira.

Masika amesema mafanikio hayo pia yanachangia utekelezaji wa sera ya elimu na mafunzo ya mwaka 2023 na malengo ya muda mrefu ya maendeleo ya taifa kuelekea Tanzania Development Vision 2050, hasa katika kuimarisha rasilimali watu wenye ujuzi.

Amesisitiza kuwa taasisi hiyo itaendelea kuimarisha mifumo ya ubora, kufanya tathmini za mara kwa mara na kushirikiana na wadau mbalimbali ili kuhakikisha elimu ya ufundi na teknolojia nchini inaendelea kukidhi viwango vya kimataifa.













Top News