Naibu Waziri wa Afya, Dkt. Florence Samizi, leo Aprili 17, 2026 ameipokea Kamati ya Ustawi wa Jamii ya Baraza la Wawakilishi Zanzibar iliyofanya ziara ya mafunzo na kubadilishana uzoefu na taasisi mbalimbali za sekta ya afya Tanzania Bara.

Ziara hiyo imehusisha kutembelea Makao Makuu ya Wizara ya Afya, Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA), Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali, Hospitali ya Taifa Muhimbili pamoja na Bohari ya Dawa (MSD).

Akiongea mara baada yakuwapokea, Dkt. Samizi amesema Serikali chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kufanya uwekezaji mkubwa kwenye sekta ya afya kwa lengo la kuboresha huduma za afya kwa wananchi.

Amesema kuwa juhudi hizo zimejikita kuimarisha miundombinu ya afya, upatikanaji wa dawa na vifaa tiba pamoja na kuboresha huduma za kibingwa na ubingwa bobezi nchini.

Kwa upande wake, Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Nasra Nassor, amesema ziara hiyo imekuwa na manufaa makubwa kwa wajumbe wa kamati kwani imewapa fursa ya kujifunza na kubadilishana uzoefu kuhusu uendeshaji wa sekta ya afya.

Ameongeza kuwa maarifa waliyoyapata yatawasaidia kuboresha utoaji wa huduma za afya Zanzibar kwa kuzingatia mifumo na mbinu walizojifunza kutoka Tanzania Bara.




Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) leo tarehe 17, Aprili 2026 amefanya kikao kazi na maafisa na askari wa Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) Makao Makuu jijini Arusha katika ukumbi wa Phase II.

Akizungumza na watumishi hao, Waziri alielekeza changamoto mbalimbali za kiutendaji zinazokabili shughuli za uhifadhi na usimamizi wa rasilimali za taasisi zitatuliwe. Vilevile, ametoa maelekezo ya namna bora ya kushughulikia na kuzitatua changamoto hizo kwa ufanisi na kwa mujibu wa sheria na taratibu zilizowekwa.

Kwenye kikao hicho Mhe. Dkt. Kijaji aliambatana na Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Hassan Abbas na Mkurugenzi wa Wanyamapori Dkt. Alexander Lobora huku akipokelewa na mwenyeji wake Kamishna wa Uhifadhi TANAPA CPA Musa Nassoro Kuji.













 

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba ameendelea kuwasisitiza Watanzania waendelee kudumisha amani nchini kwa sababu inawawezesha kushiriki katika shughuli mbalimbali za kimaendeleo.

“Tuwe makini na watu wanaohamasisha uvunjifu wa amani kwa kuwa wengine walipwa kwa vitendo hivyo. Kama wao wamechagua maisha hayo wasiiuze nchi yetu. “Lazima tulinde amani ya nchi yetu.”

 Amesema wanufaika wa kwanza wa amani ni wale wanaoishi katika eneo husika, hivyo hawana budi kuendelea kulinda amani na umoja wa kitaifa ili waendeleze shughuli mbalimbali za maendeleo.

Ameyasema hayo leo (Ijumaa, Aprili 17, 2026) alipozungumza na wananchi kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika Kona ya Mbauda akiwa katika ziara ya kikazi mkoani Arusha.

Waziri Mkuu amesisitiza hayo mara baada ya kukagua barabara ya Kilombero-Mbauda-Kisongo na Mbauda Losinyai zinazojengwa kwa njia nne pamoja na kuwekewa taa.

Ujenzi wa barabara hizo zenye jumla ya urefu wa kilomita 13 ni miongoni mwa maandalizi ya Mashindano ya Mpira wa Miguu ya Mataifa ya Afrika (AFCON), 2027 ambapo Tanzania ni mwenyeji.

Kwa upande wake, Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega amesema kuwa ujenzi wa barabara hizo unakwenda kuwasaidia wananchi wa Arusha pamoja na Watanzania kwa ujumla.

Waziri Ulega amesema mbali na kurahisisha usafiri na usafirishaji wa watu na mizigo, barabara hizo zinakwenda kuondoa tatizo la mafuriko katika baadhi ya maeneo baada ya kujengwa mitaro mikubwa.

 Pia, Waziri Ulega amesema kila baada ya kilomita moja ya barabara kutawekwa taa ambazo zitawawezesha wananchi wa maeneo hayo kuendelea na shughuli za kiuchumi usiku na mchana.

 Amemshukuru Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuidhinisha shilingi bilioni 27 ambapo kati yake bilioni 17 kwa ajili ya mkandarasi na bilioni 10 fidia kwa waliopisha mradi huo.

Naye, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda ametumia fursa hiyo kuishukuru Serikali kutokana na miradi ya maendeleo ya wananchi inayotekelezwa katika jiji hilo.

 Waziri Makonda ambaye ni mbunge wa Arusha Mjini ametaja miradi hiyo kuwa ni pamoja na ujenzi wa barabara za njia nne na uwekaji wa taa ambazo zinakwenda kurahisisha ufanyaji wa biashara.








Jeshi la Polisi Mkoa wa Morogoro linamshikilia Charles Hirali Msangi (34) kwa tuhuma za kusababisha ajali iliyosababisha abiria 57 kunusurika kifo katika eneo la Mikumi, kando ya barabara kuu ya Mikumi–Ifakara.

Ajali hiyo ilitokea Aprili 16, 2026, ambapo basi lenye namba za usajili T 289 EAG lililokuwa likiendeshwa na mtuhumiwa huyo liliacha njia na kupinduka kutokana na mwendo wa hatari.

Basi hilo lilikuwa likitoka Ifakara kuelekea Dar es Salaam likiwa na jumla ya abiria 57.

Kutokana na ajali hiyo, abiria 13 walijeruhiwa na kupatiwa matibabu katika vituo vya afya vilivyo karibu.

Jeshi la Polisi limetoa wito kwa madereva wote kuzingatia sheria na kanuni za usalama barabarani ili kuzuia ajali zinazoweza kuepukika.

Imeandaliwa na Farida Mangube.


VIWANDA vitatu vya bidhaa za Twyford vinavyofanya kazi chini ya KEDA (T) Ceramics Co. Ltd, vinavyojumuisha uzalishaji wa vigae na kioo, vinaendelea kutoa mchango mkubwa katika maendeleo ya viwanda nchini Tanzania. Kiwanda cha vigae kipo Chalinze, huku viwanda viwili vya kioo vikiwa Mkuranga. Kwa pamoja, viwanda hivi vinaajiri zaidi ya wafanyakazi 3,000 wa Kitanzania. Kupitia matumizi ya teknolojia ya kisasa ya uzalishaji wa kiotomatiki, viwanda hivi vinazalisha bidhaa bora, imara na za kudumu.

Mbali na kuboresha maisha ya wafanyakazi kupitia ajira na fursa za kiuchumi, viwanda hivi pia vinachangia maendeleo ya jamii zinazovizunguka. Aidha, bidhaa zinazozalishwa zina mchango mkubwa katika kubadilisha sekta ya ujenzi kwa kutoa vifaa vya viwango vya juu vinavyoimarisha uimara na kuongeza mvuto wa majengo, hivyo kuboresha mandhari ya mazingira kwa ujumla. Hayo yamebainishwa na Manager: Biashara na Miradi wa kampuni hiyo John Chimwejo, alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hii, mjini Mkuranga, mkoani Pwani, hivi karibuni.
Muonekano kwa juu (Overview) ya kiwanda cha vioo (glass) cha kampuni ya KEDA (T) Ceramics Co. Ltd kinachozalisha vioo vya Twyford Glass kilichopo eneo la Msufini, Kidete Mbezi, wilaya ya Mkuranga, mkoani Pwani.

Bwana Chimwejo amesema kuwa ushahidi wa mandhari nzuri ya majengo yaliyopendeza kwa vigae na vioo vya Twyford unaonekana wazi ukitembelea maeneo mbalimbali nchini Tanzania. Katika hospitali, shule, pamoja na majengo ya serikali, taasisi za umma na binafsi, majengo mengi ya kisasa yamepambwa na vigae na vioo vya Twyford vinavyoboresha muonekano wake kwa kiasi kikubwa.

Kabla ya uwepo wa viwanda hivi nchini, vifaa vingi vya ujenzi kama vigae na vioo kwa majengo makubwa vilikuwa vikiagizwa kutoka nje ya nchi. Hata hivyo, kwa sasa vinazalishwa ndani ya Tanzania kupitia viwanda vya Twyford, hatua ambayo imechangia kupunguza gharama za ujenzi kwa kiasi kikubwa. Aidha, uzalishaji wa ndani umefanya vifaa hivi kupatikana kwa gharama nafuu huku ubora ukiendelea kuwa wa hali ya juu. Wafanyakazi wa kiwanda cha vioo (glass) cha kampuni ya KEDA (T) Ceramics Co. Ltd kinachozalisha vioo (float glass) vya Twyford kilichopo eneo la Msufini, Kidete Mbezi, wilaya ya Mkuranga, mkoani Pwani. Ajira pia inazingatia usawa wa kijinsia, hakuna kazi ya kiume, wala kazi ya kike, kwao kazi ni kazi.



Bwana Chimwejo ametolea mfano wa Wodi ya Watoto Wachanga katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili jijini Dar es Salaam ambayo sakafu safi na ang’avu zilizowekwa vigae vya ubora wa juu vya Twyford. Hata katika Hospitali ya Rabininsia iliyopo Tegeta, vigae vinavyotumika ni vya Twyford. Aidha, vigae vya Twyford vimewekwa katika Jengo la Halmashauri ya Mji wa Mbinga Kusini, na kulifanya jengo hilo la ofisi ya serikali kuwa na muonekano wa kisasa na wa kuvutia.

Chimwejo ametaja Eneo la Viwanda la Chalinze, lililopo kilomita 70 kutoka jijini Dar es Salaam, ndipo kilipo kiwanda cha kisasa cha vioo na vigae vya Twyford kinachofanya kazi kwa saa 24, kikizalisha vigae kwa ajili ya soko la Tanzania na soko la nchi za Afrika.



Mbali na kiwanda kilichopo Chalinze, viwanda vingine viwili vya kioo vipo umbali wa takribani kilomita 100 kutoka Dar es Salaam katika maeneo ya Mbezi, Kidete Msufini na Mkiu, Nyamato, Wilaya ya Mkuranga, ambapo viwanda hivyo vikubwa vya kioo vinafanya kazi kwa ufanisi mkubwa. Viwanda hivi vinatumia tanuru zenye joto la zaidi ya nyuzi joto 1,000 za Selsiasi, ambapo kioo kilichoyeyushwa huundwa kuwa mabamba ya maumbo mbalimbali kupitia mitambo ya kisasa inayojiendesha kwa mfumo wa otomatiki unaodhibitiwa na kompyuta. Bidhaa za Twyford Glass hazitumiki tu katika miradi ya ujenzi ndani ya Tanzania, bali pia husafirishwa kwenda masoko mbalimbali ya nje ya nchi.

Akizungumzia historia ya viwanda hivyo, Manager: Biashara na Miradi wa kampuni hiyo John Chimwejo, amesema kiwanda cha uzalishaji wa vigae vya Twyford nchini Tanzania kilianza uzalishaji mwaka 2017, na kuongeza uwekezaji kwa kasi, ndani ya miaka michache tu, kimeanzisha vituo vya uzalishaji vinavyohusisha sekta zote mbili za kauri na kioo, sio tuu kwa matumizi ya soko la Tanzania pekee, bali soko la Afrika Mashariki, Afrika nzima na nje ya Afrika.

Mtaalamu wa Kichina na wataamu wazalendo wa Kitanzania, wakiwa kwenye chumba cha kuendeshea mitambo ya uzalishaji vioo (Control room) inayojiendesha yenyewe ki atomatikali (automated) kwa kutumia compyuta kuzalisha vioo (float glass) kwenye kiwanda cha KEDA (T) Ceramics Co. Ltd kilichopo eneo la Mbezi wilaya ya Mkuranga, mkoani Pwani.



Viwanda hivi vitatu vya kisasa vya vifaa vya ujenzi, vimejenga msingi muhimu kwa sekta ya ujenzi, kwa upatikanaji wa vifaa bora, imara na vya gharama nafuu kwa Tanzania na nchi za Afrika ambapo, zamani vifaa hivi viliagizwa kutoka nje ya nchi. Bidhaa hizi husambazwa si tu kwa soko la ndani la Tanzania lakini pia husafirishwa kwenda nchi kadhaa ikiwa ni pamoja na Madagaska, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Rwanda, Uganda, Malawi, Sudan Kusini, Afrika Kusini, na Mauritius, na kuifanya chapa ya Twyford, kuwa ni chapa yenye ushawishi mkubwa wa vigae na vioo kwa Tanzania, Afrika Mashariki na kwingine Afrika.

Leo, Twyford Tanzania inaendesha viwanda vitatu vya uzalishaji nchini Tanzania, ikiwa na kiwanda kimoja cha vigae na viwanda viwili vya kioo. Kiwanda cha uzalishaji wa vigae kilichopo Chalinze kina ukubwa wa takribani hekta 93 na kimeajiri karibu wafanyakazi 1,000. Kiwanda hiki kimewekewa mitambo ya kisasa ya uzalishaji inayojiendesha kwa mfumo wa otomatiki, inayowezesha uzalishaji wa kiwango kikubwa kwa muda mfupi. Mchakato wa uzalishaji huanzia usindikaji wa malighafi, ukandamizaji, uchomaji hadi ufungashaji wa bidhaa.



Viwanda viwili vya uzalishaji wa vioo vya Twyford Tanzania vilivyopo Mbezi na Nyamato, Wilaya ya Mkuranga mkoani Pwani, vina ukubwa wa takribani hekta 120 kwa pamoja na vimeajiri zaidi ya wafanyakazi 2,000. Viwanda hivi huzalisha vioo vya ubora wa hali ya juu, vyenye uwezo wa kuyeyusha zaidi ya tani 1,100 za malighafi ya kioo kila siku. Vinazalisha aina mbalimbali za vioo vya ujenzi kwa unene na maumbo tofauti kuanzia milimita 3 hadi 12, ikiwa ni pamoja na kioo cha kawaida (clear glass), kioo chenye rangi, kioo kinachoakisi mwanga, pamoja na aina nyingine za vioo vya matumizi mbalimbali.

Kutokana na ubora wa bidhaa na uwezo mkubwa wa uzalishaji, Vioo vya Twyford husafirishwa kwenda zaidi ya nchi na maeneo 43 duniani, yakiwemo Afrika Mashariki, Afrika Kaskazini, Afrika Kusini, Mashariki ya Kati, Amerika na Ulaya.

Ndani ya Tanzania, Twyford Tanzania imeanzisha mtandao wa mauzo wa kitaifa, kuanzia Dar es Salaam, Dodoma hadi mikoa mingine, ikifikia miji, maeneo ya vijijini, na hata visiwa vya Zanziba na Pemba. Kampuni hiyo inafanya yote haya ili kuhakikisha kwamba vifaa bora vya ujenzi vinapatikana kwa urahisi zaidi kuwahudumia watumiaji wa ndani na nje ya nchi. Twyford Tanzania pia imetoa faida kubwa za kiuchumi kwa Tanzania. Kwa upande mmoja, biashara hiyo inachangia mapato makubwa ya kodi kwa serikali kila mwaka; kwa upande mwingine, inazalisha mapato muhimu ya fedha za kigeni kupitia mauzo ya bidhaa nje ya nchi.

Hii inayofanywa na viwanda vya vigae na vioo vya Twyford Tanzania inaweza kuonekana kwa jicho la kawaida kama ni uzalishaji wa vifaa vya ujenzi tu. Hata hivyo, kwa mtazamo mpana na wa kina, Twyford Tanzania haizalishi tu vifaa vya ujenzi, bali inachangia kwa kiasi kikubwa kubadilisha taswira ya uchumi wa Tanzania.

Baadhi ya wanafunzi wa Shule ya Sekondari Mkiu wakiwa katika picha ya pamoja baada ya kupokea msaada wa madawati, viti na vitabu uliotolewa na KEDA (T) Ceramics Co. Ltd kwa lengo la kuboresha mazingira yao ya kujifunzia.

Kampuni hii inasaidia kuihamisha Tanzania kutoka kuwa nchi inayotegemea uagizaji wa bidhaa kutoka nje (import-dependent country) hadi kuwa nchi inayozalisha na kusafirisha bidhaa nje (export-oriented country), na hivyo kuwa kitovu cha uzalishaji wa vifaa vya ujenzi vinavyouzwa katika masoko ya kimataifa. Kupitia mabadiliko haya, taifa linapata ongezeko la mapato ya fedha za kigeni na kuimarisha uchumi wa nchi kwa ujumla.

Kwa miaka mingi, Twyford Tanzania imeendelea kuboresha teknolojia yake ya uzalishaji kupitia uboreshaji wa ubunifu wa michanganyiko ya malighafi na kuimarisha mifumo ya udhibiti wa ubora. Hatua hizi zimechangia kwa kiasi kikubwa kuongeza ubora na ufanisi wa bidhaa zake. Wakati huohuo, kampuni imeongeza matumizi ya malighafi zinazopatikana ndani ya nchi, jambo ambalo limepunguza gharama za uzalishaji na kupunguza utegemezi wa uagizaji wa malighafi kutoka nje ya nchi. Hii ni faida kubwa kwa taifa, kwani inasaidia kuongeza uzalishaji wa ndani unaotegemea rasilimali za nchini.



Ukiondoa faida kwa Tanzania na Watanzania kutokana na upatikanaji wa bidhaa bora, zenye ubora wa juu na gharama nafuu kutoka viwanda vya Twyford Tanzania, uwepo wa viwanda hivi pia umechangia kwa kiasi kikubwa katika ajira kwa Watanzania waliopata ajira rasmi katika shughuli za uzalishaji.

Menejiment ya ya kiwanda cha KEDA (T) Ceramics Co. Ltd wakiwa na wajumbe wa serikali ya kijiji Gongoni , waalimu, wazazi na wanafunzi wa Shule ya Gongoni, wilayani Mkuranga, mkoani Pwani, baada ya kukabidhi vifaa vya shule na vigae kwa serikali ya kijiji hicho kusaidia ujenzi wa shyule ya sekondari ya Gongoni.

Aidha, mamia kwa maelfu ya Watanzania wananufaika kupitia mnyororo wa thamani ikiwemo usambazaji, uuzaji na ununuzi wa bidhaa hizo bora. Zaidi ya hayo, jamii zinazozunguka viwanda hivi zimeendelea kunufaika kupitia utekelezaji wa sera ya uwajibikaji kwa jamii (CSR), ambayo imekuwa ikiunga mkono maendeleo ya kijamii na kuboresha maisha ya wananchi wa maeneo husika.


WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, amewataka Watanzania kuendelea kudumisha amani na utulivu nchini akisisitiza kuwa mazingira ya amani ndiyo msingi muhimu unaowawezesha wananchi kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo na kukuza uchumi wa taifa.

Amesema ni muhimu kwa wananchi kuwa makini na watu wanaohamasisha uvunjifu wa amani, akibainisha kuwa baadhi yao hufanya hivyo kwa maslahi binafsi. Alionya kuwa watu hao wasiruhusiwe kuihatarisha nchi, akisisitiza kuwa ni wajibu wa kila Mtanzania kulinda amani iliyopo.

Dkt. Nchemba ameeleza kuwa wanufaika wakuu wa amani ni wananchi wenyewe, hivyo wanapaswa kuilinda kwa nguvu zote ili kuendeleza shughuli zao za kila siku, ikiwa ni pamoja na biashara, kilimo na uwekezaji unaochangia maendeleo ya jamii.

Ameyasema hayo leo Ijumaa, Aprili 17, 2026, alipokuwa akizungumza na wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika Kona ya Mbauda mkoani Arusha, ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya kikazi ambapo pia alikagua maendeleo ya ujenzi wa barabara muhimu jijini humo.

Aidha, ameeleza kuwa ujenzi wa barabara za Kilombero–Mbauda–Kisongo na Mbauda–Losinyai zenye urefu wa kilomita 13 ni sehemu ya maandalizi ya mashindano ya AFCON 2027, huku Serikali ikiendelea kuboresha miundombinu ili kurahisisha usafiri, kukuza biashara na kuhakikisha wananchi wananufaika na fursa za kiuchumi zinazotokana na miradi hiyo.



Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, ambaye ni Mwakilishi wa Ngazi ya Juu wa Mwenyekiti wa Kamisheni ya Umoja wa Afrika kwenye Eneo la Pembe ya Afrika na Bahari ya Shamu jana amekutana na kufanya mazungumzo na Rais William Ruto wa Kenya, Nairobi. 
Picha na IKULU, NAIROBI

RAIS Mstaafu Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, ambaye ni Mwakilishi wa Ngazi ya Juu wa Mwenyekiti wa Kamisheni ya Umoja wa Afrika kwenye Eneo la Pembe ya Afrika na Bahari ya Shamu jana amekutana na kufanya mazungumzo na Rais William Ruto wa Kenya, Nairobi.

Pamoja na mambo mengine, viongozi hao walipata fursa ya kuzungumzia mchakato wa kutafuta amani nchini Sudani Kusini, hususan kwa kuzingatia nafasi ya Kenya katika mgogoro wa nchini huo.

Moja ya jitihada za kuleta amani nchini Sudani kusini zimefanywa na Serikali ya Kenya kupitia Mpango wa Amani wa Tumaini ambao umelenga kuvijumuisha katika mazungumzo ya amani vikundi vyote vya kijamii na vya kijeshi ambavyo havikutia saini katika Makubaliano ya Amani nchini Sudani Kusini R-ARCSS yaliyosainiwa Mwaka 2018.

Ziara hii ya Rais Mstaafu Dkt. Kikwete ni sehemu ya kutekeleza kujumu lake jipya la kuwa mpatanishi wa amani nchini Sudani Kusini, ambapo tangu kuteuliwa kwake ameweza kukutana na Viongozi mbalimbali wenye ufuasi katika hali ya amani, ulinzi na usalama nchini Sudani kusini wakiwemo Rais Cyril Ramaphosa wa Afrika Kusini, Rais Yoweri Museveni wa Uganda na sasa Rais William Ruto wa Kenya.

Aidha, Dkt. Kikwete ameshafanya ziara nchini Sudani Kusini na kukutana na Makundi yote muhimu katika mgogoro huo kwa lengo la kukubaliana mkakati endelevu utakaohakikisha amani inarejea katika nchi hiyo changa kuliko zote barani Afrika

Mwandishi wetu.
MWAKILISHI wa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzani Mussa Azzan Zungu, Bi.Hellen Madanganya, amewapongeza walimu pamoja na wanafunzi wa Shule ya Sekondari Kibasila kwa kuendelea kufanya vizuri kwenye mitihani yao ya awamu zilizopita na kuwatia moyo kuwa kutokana na umakini alionao Spika Mussa Azzan Zungu, changamoto zote zilizotajwa kwenye mahafari hayo anaamini atazifanyika kazi huku akiwataka wanafunzi hao kuiga mifano na kufanya vizuri zaidi kwenye mitihani ijayo .

Katibu Madanganya aliyasema hayo Jijini Dar es Salaam jana wakati wa mahafari ya 26 ya Kidato cha sita yaliyofanyika kwenye Viwanja vya Shule hiyo ambapo wanafunzi waliyofanya mahafari hayo walikuwa ni 314, wasichana 145 na wavulana 169.

Alisema kuwa amepokea taarifa za changamoto zilizosomwa kwenye risala ya Mkuu wa Shule hiyo Juma Boniface Orenda na kusema kuwa yeye akiwa Mwakilishi wa Spika atafikisha ujumbe huo na anaamini utafanyiwa kazi na kusema kuwa yeye hataweza kujibu risala hiyo badala yake ataifikisha kwa Spika jinsi ilivyo.

“Mimi nipo kwa Itifaki ya Spika kwa maana ya kwamba ni mwakilishi, lakini ninapenda kuwahakikishia kwamba Spika wetu ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Ilala ni mtu makini sana ambaye ninaamini yote haya ataenda kuyashughulikia kwa haraka zaidi,” alisema Kiongozi huyo.


Mkuu wa Shule hiyo ya Sekondari Kibasila Dkt. Juma Orenda, alisema kuwa pamoja na mafanikio makubwa waliyoyapata hasa kwenye ufaulu mkubwa wa wanafunzi waliopita lakini wamekuwa wakipokea maelekezo mbalimbali ya kiserikali na kuyafanyia kazi likiwemo suala kubwa la kuzitaka shule zote kuhakikisha wanafunzi wanapata chakula mashuleni na kusema kuwa suala hilo wamelikamilisha kwa asilimia 100 na kwamba watoto wanapata chakula na kwa wakati.

“Tunatanguliza shukrani zetu za dhati kwa Ofisi ya Spika wa Bunge na Mbunge Jimbo la Ilala Mussa Azzan Zungu kwa kutambua mwaliko wetu na kututumia mwakilishi wake Bi. Madanganya, hili ni jambo kubwa sana na la kufurahisha,” lakini pia kupitia kwa kiongozi huyu nipende kusema kuwa tunazo changamoto mbalimbali kubwa ikiwa ni pamoja na ile ya kutokuwa na gari maalumu inayoweza kutusaidia pindi tu inapotokea changamoto za kiafya,” alisema.

Dkt. Orenda, alisema pia changamoto nyingine ambayo shule hiyo imekuwa ikikabiliana nayo ni pamoja na kutokuwa na Sehemu ya wanafunzi kulia chakula kwa wakati na kwa pamoja (Cantiini), kutokuwa na dhamani za kutosha kama meza na vitu.

“Lakini pia Mhe. Tunayochangamoto nyingine ambayo ni kwa watu wenye ulemavu ambao pia wamekuwa na changamoto ya kutokuwa na fimbo nyeupe, komputa mpakato na vitendea kazi vingine,” alisema.

Wataalam kutoka Makumbusho ya Taifa la Tanzania wametoa mafunzo ya kizalendo kwa washiriki wa shindano la Urembo wa Dunia, Tanzania (Miss World Tanzania 2026) katika ukumbi wa White Sand Resort, tarehe 16/04/2026 ikiwa ni sehemu ya kuwajengea uelewa kuhusu Utalii, historia, utamaduni na urithi wa Taifa.

Katika mafunzo hayo, mada mbalimbali ziliwasilishwa na wakufunzi hao kwa lengo la kuwawezesha washiriki kuitambua historia yao na kuwa mabalozi bora wa utamaduni wa Tanzania ndani na nje ya nchi.

Afisa Utalii, Bw. Chance Ezekiel aliwasilisha mada kuhusu Utalii wa Tanzania, akieleza kwa kina hatua za maendeleo ya sekta hiyo na kutoa mwelekeo wa kitaifa kuhusiana na tasnia nzima ya utalii na ubalozi wake hapa Tanzania.

Kwa upande wa Wahifadhi Historia, Bw. Nasri Omari alitoa mada kuhusu historia ya Makumbusho ya Taifa kwa kutolea ufafanuzi wa mamlaka na maeneo ya kiutawa ya taasisi pamoja na vituo na Malikale zinazosimamiwa nayo. Naye Bw. Shomari Rajabu alijikita katika kuelezea maadili, mila na namna bora ya kuzungumza na jamii ili kuendeleza na kulenga kuwa mabalozi bora wa Tanzania.

Washiriki wa Miss World Tanzania 2026 walionesha kufurahishwa na mafunzo hayo, wakibainisha kuwa yameongeza maarifa na uelewa wao kuhusu Utalii, historia, mila na desturi za Mtanzania.

Makumbusho ya Taifa inaendelea kutekeleza jukumu lake la kutoa elimu kwa umma kuhusu uhifadhi na uendelezaji wa urithi wa taifa kupitia programu mbalimbali za elimu na mafunzo.








Na Joseph Mahumi, WF, Washington D.C, Marekani
Tanzania imejipanga kikamilifu kuwa kitovu cha uwekezaji barani Afrika na inawakaribisha wawekezaji wa Marekani kuchangamkia fursa lukuki zilizopo katika sekta mbalimbali za uchumi.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) wakati alipoongoza ujumbe wa Tanzania katika Mkutano wa Uwekezaji ulioandaliwa na Baraza la Biashara la Kimataifa- Business Council for International Understanding (BCIU), uliofanyika katika Ofisi za BCIU, jijini Washington D.C nchini Marekani, pembezoni mwa Mikutano ya Majira ya Kipupwe ya Benki ya Dunia na Shirika la Fedha la Kimataifa-IMF.

Mhe. Balozi Omar alieleza kuwa, Tanzania inaendelea kuimarika kiuchumi na kutoa mazingira rafiki kwa biashara na uwekezaji sambamba na uchumi wake kuendelea kukua kwa kasi, ukifikia asilimia 5.5 mwaka 2024 na unatarajiwa kufikia asilimia 6.0 mwaka 2025, hali inayochochewa na sekta muhimu kama kilimo, viwanda, madini, ujenzi pamoja na huduma za kifedha.

“Serikali inaendelea kuboresha mazingira ya biashara na kuvutia uwekezaji wa muda mrefu ili kuhakikisha sekta binafsi inachukua nafasi yake kikamilifu katika kukuza uchumi” alisema Mhe. Balozi Omar.

Aliongeza kuwa mahusiano ya kibiashara kati ya Tanzania na Marekani yanaendelea kuimarika kwa kasi, ambapo thamani ya biashara kati ya nchi hizo imefikia dola za Marekani bilioni 1.4 mwaka 2024 huku uwekezaji wa moja kwa moja kutoka Marekani umeongezeka kutoka dola milioni 12.3 mwaka 2020 hadi dola milioni 40 mwaka 2023.

Akifafanua fursa zilizopo, Mhe. Balozi Omar alisema Tanzania ina utajiri mkubwa wa madini muhimu kwa nishati safi kama graphite, nickel na madini adimu, huku akisisitiza kuwa nchi inakaribisha ubia wa kuongeza thamani badala ya kuuza malighafi pekee.

“Hatupendelei kuuza mawe ghafi, bali tunakaribisha ushirikiano wa kuanzia uchimbaji hadi uzalishaji wa bidhaa za mwisho zenye thamani kubwa, na Tanzania ina soko kubwa la vijana wanaohitaji huduma za kidijitali, hivyo ni fursa adhimu kwa wawekezaji wa teknolojia pia,” alisema Mhe. Balozi Omar.

Aidha, alisema kuwa katika sekta ya kilimo, Tanzania inalenga kuwa ghala la chakula kwa Afrika na dunia, akihimiza uwekezaji katika kilimo cha kisasa na usindikaji wa mazao. Pia alieleza kuwa sekta ya afya, miundombinu na maeneo maalum ya uwekezaji (SEZs) yana fursa kubwa kutokana na mahitaji makubwa ya soko la ndani na kikanda.

Naye Balozi wa Tanzania nchini Marekani, Mhe. Dkt. Elsie Sia Kanza alisema kuwa mkutano huo na wawekezaji wa Marekani ni jitihada za kuvutia zaidi mitaji kutoka Marekani kupitia Diplomasia ya kiuchumi.

Alisema kuwa Tanzania inaanza kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050 ambayo imeelekeza nchi iweze kufikia uchumi wa dola za Marekani trilioni 1 ifikapo Mwaka 2050 na kwamba uwekezaji wa Sekta Binafsi unatarajiwa kuwa na mchango mkubwa.

Kwa upande wa wawekezaji walioshiriki mkutano huo ulioongozwa na Rais na Afisa Mtendaji Mkuu wa Baraza la Biashara - Business Council for International Understanding (BCIU), Bw. Peter Tichansky, walisema wameona kuna fursa za kiuchumi nchini Tanzania na wamejipanga kuwekeza katika sekta muhimu ikiwemo kilimo, madini, afya, miundombinu ya bandari, Teknolojia ya Habari na Mawasiliano pamoja na Bima ya wakulima.

Walisema kuwa eneo pamoja na maeneo hayo mengine, wanataka kuwekeza katika kilimo kwa kuzalisha mbegu bora pamoja na kuwawekea wakulima bima ya kilimo ili wawe na uhakika wa kuendesha shughuli zao bila kupata hasara ya majanga yatokanayo na changamoto mbalimbali.


Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akizungumza jambo wakati wa MKutano wa Uwekezaji ulioandaliwa na Baraza la Biashara - Business Council for International Understanding (BCIU), uliofanyika katika Ofisi za BCIU, jijini Washington D.C nchini Marekani, pembezoni mwa Mikutano ya Majira ya Kipupwe ya Benki ya Dunia na Shirika la Fedha la Kimataifa-IMF, ambapo BCIU wameonesha nia kuwekeza nchini katika Bima kwa wakulima, kuzalisha mbegu bora za kisasa, bandari na katika Sekta ya Afya.
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb)(kushoto), akiwa na Rais na Afisa Mtendaji Mkuu wa Baraza la Biashara - Business Council for International Understanding (BCIU), Bw. Peter Tichansky, baada ya Mkutano wao wa Uwekezaji ulioandaliwa na Baraza la Biashara - Business Council for International Understanding (BCIU), uliofanyika katika Ofisi za BCIU, jijini Washington D.C nchini Marekani, pembezoni mwa Mikutano ya Majira ya Kipupwe ya Benki ya Dunia na Shirika la Fedha la Kimataifa-IMF, ambapo BCIU wameonesha nia kuwekeza nchini katika Bima kwa wakulima, kuzalisha mbegu bora za kisasa, bandari na katika Sekta ya Afya.
Ujumbe wa Tanzania ukiongozwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (kulia), ukiwa katika Mkutano wa Uwekezaji ulioandaliwa na Ujumbe Baraza la Biashara - Business Council for International Understanding (BCIU) (kushoto), uliofanyika katika Ofisi za BCIU, jijini Washington D.C nchini Marekani, pembezoni mwa Mikutano ya Majira ya Kipupwe ya Benki ya Dunia na Shirika la Fedha la Kimataifa-IMF, ambapo BCIU wameonesha nia kuwekeza nchini katika Bima kwa wakulima, kuzalisha mbegu bora za kisasa, bandari na katika Sekta ya Afya.
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (Katikati), Rais na Afisa Mtendaji Mkuu wa Baraza la Biashara - Business Council for International Understanding (BCIU), Bw. Peter Tichansky (wa tatu kulia), Balozi wa Tanzania nchini Marekani, Mhe. Elsie Sia Kanza (wa pili kulia), Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Mipango ambaye pia ni Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Mipango, Dkt. Tausi Kida (wa pili kushoto), Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango Zanzibar, Bw. Aboud Hassan Mwinyi (wa tatu kushoto), na viongozi wengine wa BCIU, Bw. Mathias Berninger (wa kwanza kulia) na Bi. Mesiya Mwangoka (kushoto), wakiwa katika picha ya pamoja baada ya MKutano wa Uwekezaji ulioandaliwa na Baraza la Biashara - Business Council for International Understanding (BCIU), uliofanyika katika Ofisi za BCIU, jijini Washington D.C nchini Marekani, pembezoni mwa Mikutano ya Majira ya Kipupwe ya Benki ya Dunia na Shirika la Fedha la Kimataifa-IMF, ambapo BCIU wameonesha nia kuwekeza nchini katika Bima kwa wakulima, kuzalisha mbegu bora za kisasa, bandari na katika Sekta ya Afya.

(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, WF, Washington D.C, Marekani)

Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma 

Serikali ya Tanzania kupitia Mamlaka ya Serikali Mtandao (e-GA) imeweka mkazo katika kuimarisha usalama wa mifumo ya TEHAMA, kuongeza ufanisi wa huduma za kidijitali pamoja na kuunganisha mifumo ya taasisi za umma ili kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.

Akizungumza Bungeni jijini Dodoma Aprili 17, 2026, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Ridhiwani J. Kikwete, alisema hatua hizo ni sehemu ya mpango wa maboresho ya huduma za serikali kwa mwaka wa fedha 2026/27.

Waziri Kikwete alieleza kuwa katika kipindi hicho, e-GA itafanya tathmini ya usalama wa mifumo na miundombinu ya TEHAMA katika taasisi 571 za umma ili kuhakikisha mifumo hiyo inafanya kazi kwa ufanisi, uimara na usalama wa hali ya juu.

Aidha, Serikali inalenga kuboresha na kuunganisha mifumo jumuishi ya TEHAMA pamoja na mifumo ya kisekta na ya kitaasisi, lengo likiwa ni kupunguza urudufu wa mifumo na kuongeza ushirikiano kati ya taasisi za serikali.

Katika hatua nyingine, e-GA itahusika katika kuchambua, kubuni na kuendeleza mifumo mipya ya kisekta kwa taasisi mbalimbali, ili kurahisisha utoaji huduma na kuongeza ufanisi wa kiutendaji ndani ya serikali.

Serikali pia imepanga kuunganisha taasisi zote za umma kupitia Mfumo wa Kubadilishana Taarifa Serikalini (GovESB), hatua itakayorahisisha mawasiliano na ushirikiano wa kidijitali kati ya taasisi.

Vilevile, juhudi zitaelekezwa katika kuimarisha tafiti na ubunifu wa teknolojia mpya za TEHAMA ili kuibua huduma bora zaidi kwa wananchi, sambamba na kuhakikisha matumizi salama ya teknolojia zinazoendelea kujitokeza duniani.

Katika kuboresha upatikanaji wa huduma, mtandao wa mawasiliano wa Serikali utapanuliwa hadi kufikia wilaya zote nchini, huku mifumo kama e-Office na huduma nyingine za kidijitali ikiendelea kuboreshwa.

Kwa upande wa miundombinu, e-GA itaendelea kusimamia vituo vya kuhifadhi data za Serikali pamoja na mifumo ya ulinzi dhidi ya majanga ya kimtandao ili kuhakikisha taarifa za serikali zinalindwa wakati wote.

Aidha, Serikali itatoa mafunzo kwa watumishi wa umma na watumiaji wa mifumo ya TEHAMA ili kuongeza uelewa na ufanisi katika matumizi ya teknolojia katika utumishi wa umma.

Kwa ujumla, maboresho hayo yanalenga kuimarisha utawala bora wa kidijitali, kupunguza gharama za uendeshaji wa serikali na kuongeza kasi ya utoaji wa huduma bora kwa wananchi.



● Shughuli za Uzinduzi wake Mkubwa na wa Kihistoria Kufanyika Katika Hifadhi ya Taifa ya Serengeti

Serengeti Premium Apple, bidhaa ya kampuni ya Serengeti Breweries Limited (SBL), imekuwa kinywaji cha kwanza tayari kunyweka au Ready-to-Drink (RTD) kilichotengenezwa hapa nchini Tanzania. Kikiwa na asili ya Kitanzania, chapa hii inaleta ladha ya kipekee na hadhi ya juu, iliyobuniwa kuakisi ndoto, mafanikio, na ari ya kusherehekea ya Mtanzania wa kisasa.

Ikiwa na mojawapo ya jina la maeneo mashuhuri duniani, Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, uzinduzi wa chapa hii unatarajiwa kufanyika katika mandhari halisi na ya kuvutia ya hifadhi hiyo, ukichanganya uzoefu wa kipekee na ladha ya kipekee wa kinywaji hiki.

Akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi huo wa kipekee, Mkurugenzi Mtendaji wa SBL, Obinna Anyalebechi, alielezea mafanikio hayo kama hatua muhimu kwa kampuni katika kuleta kinywaji cha kwanza cha hadhi ya juu na ladha ya kipekee tayari kunyweka kilichotengenezwa nchini.

 Alisisitiza kuwa chapa hiyo imeundwa kukidhi mahitaji ya watumiaji wanaotafuta ladha mpya, nyepesi, na yenye kuburudisha, huku pia ikiziba pengo la hadhi na usasa katika soko.

“Kwetu SBL, tunabuni bidhaa kuendana na mahitaji ya watumiaji wetu. Tunawasikiliza kwa makini, wanachotaka na namna wanavyotaka kusherehekea nyakati zao muhimu. Hitaji la kuwa na chapa ya nchini, inayojivunia Utanzania na kuakisi hadhi na usasa, ilikuwa dhahiri. Ndiyo maana leo tunazindua Serengeti Premium Apple kukidhi matarajio hayo.

Hiki siyo tu kinywaji, bali ni ishara ya mwelekeo wa Tanzania. Mtumiaji wa leo hanywi tu, anatengeneza kumbukumbu muhimu za maisha. Zaidi ya hayo, uzalishaji wa ndani unachangia kukuza sekta ya viwanda, kuimarisha mnyororo wa thamani, kuzalisha ajira, na kuthibitisha kuwa bidhaa za Tanzania zinaweza kushindana kimataifa,” alisema Anyalebechi

Uzinduzi wa Serengeti Premium Apple katika Hifadhi ya Serengeti unadhihirisha fahari ya rasilimali za Tanzania, ukionyesha kuwa hadhi na ubora wa hali ya juu hauhitaji kuagizwa kutoka nchi zingine.

 Kinywaji hiki kinaweza kufurahiwa katika mazingira ya kifahari kama vile migahawa au bustani nzuri, kikiwa ni cha nyumbani, cha kujivunia, na kilichobuniwa kwa ladha ya kipekee.

Kwa kuchagua Hifadhi ya Serengeti kama sehemu ya kufanyia uzinduzi, SBL pia imewekeza kimkakati katika sekta ya utalii, ikiiweka Tanzania kwenye ramani ya kimataifa na kuwahamasisha Watanzania kuendelea kuvumbua hazina ya vivutio walivyonavyo.

Kupitia ushiriki wa watengeneza maudhui wakubwa watakaorekodi kila hatua ya tukio, ambapo Serengeti ndiyo mhusika mkuu wa hadithi hii. Picha, video, na simulizi zinabeba ujumbe mmoja mkubwa, kwamba hadhi ya Mtanzania wa kisasa inatoka ndani ya nchi, siyo kuazimwa au kuagizwa, na hii ndiyo fahari halisi ya chapa hii mpya.

Akizungumzia uzinduzi huo, Mkurugenzi wa Ubunifu na Masoko wa SBL, Henry Esiaba, alisema: “Tunajivunia kuzindua bidhaa hii katika Hifadhi ya Serengeti, ambapo tumewaleta pamoja wanawake wenye ushawishi, watengeneza maudhui na wabunifu kutoka sekta mbalimbali, na sauti halisi za utamaduni wetu katika moja ya maeneo ya kuvutia zaidi duniani, huu si uzinduzi wa kawaida, bali ni kusherehekea kile ambacho Tanzania inaweza kutengeneza.

Serengeti ndiyo chimbuko la hadithi ya chapa hii. Kuwapeleka wabunifu hawa wa maudhui kwenye hifadhi ni mwaliko kwetu sote kuendelea kuvumbua ladha na fahari ya Tanzania. Hawatohudhuria tukio pekee, bali pia wataiishi chapa na kupata fursa ya kuwepo eneo ambalo imeanzia. 

Kwa kufanya hivyo, watakuwa mabalozi wa kwanza kushiriki uzinduzi wa aina yake na kipekee kuwahi kutokea nchini: Sophistication. Bottled.”

Akitoa mtazamo wake kama balozi wa chapa, Flaviana Matata alisema: “Kwangu mimi, ni muhimu kushirikiana na chapa inayowakilisha Tanzania ya kisasa, yenye ujasiri, kujiamini, na mtazamo wa kusonga mbele. 

Ushirikiano huu ni kuhusu kusimulia hadithi na kuunganisha watu. Tunataka kila mtu ajione kuwa ni sehemu ya chapa hii. Na huu ni mwanzo tu, mahali popote pale ambapo watakuwa wakifurahia nyakati nzuri, Serengeti Premium Apple itakuwepo.”

Ikiwa na ladha ya tufaa au Apple‘’ iliyo nyororo, yenye kuburudisha na utamu wa kiwango cha juu, Serengeti Premium Apple imetengenezwa maalum kwa nyakati mbalimbali za kufurahia maisha, kuanzia mapumziko ya jioni na marafiki mpaka mitoko ya usiku na burudani tofauti jijini.

Ni ladha iliyovumbuliwa mahususi kwa Watanzania wenye ari na ndoto kubwa - ya Kujivunia ya Kitanzania, Yenye Hadhi ya Juu, na Yenye Ujasiri Usiofichika.











Top News