Mhe Mbunge wa Jimbo la Mlimba,Dkt KellenRose Rwakatare, ametembelea mabinti 300 wanaosoma katika Chuo cha Maendeleo FDC Ifakara na kuwapatia mahitaji mbalimbali muhimu kwa ajili ya kuendeleza masomo yao ya ufundi stadi.

Ziara hiyo imelenga kuwatia moyo, kuwasikiliza pamoja na kuthibitisha dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan katika kuwawezesha vijana wa kike kielimu na kiuchumi.

Akizungumza na mabinti hao, Mhe Mbunge aliwahimiza kusoma kwa bidii, kutumia vyema fursa waliyoipata na kuwa chachu ya mabadiliko katika jamii. Ziara hiyo pia ilisindikizwa na viongozi mbalimbali wa Wilaya ya Kilombero waliopongeza juhudi hizo za maendeleo




 

Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) Mkoa wa Dodoma unashiriki katika Kliniki maalum ya kutatua kero na changamoto mbalimbali za wananchi iliyoandaliwa na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, inayofanyika tarehe 3 hadi 6 Machi, 2026 katika viwanja vya Nyerere Square jijini Dodoma.

Kupitia kliniki hiyo, TBA inakutana na wateja wake ambao ni wapangaji wa nyumba zake kwa lengo la kusikiliza na kutatua changamoto pamoja na kero mbalimbali zinazojitokeza katika maeneo wanayoishi.

Aidha, kliniki hiyo imekuwa fursa kwa taasisi mbalimbali za Serikali kutoa elimu kwa wananchi pamoja na kueleza mafanikio yaliyopatikana katika utekelezaji wa majukumu yao ndani ya siku 100 za Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan tangu kuingia madarakani.

Katika kliniki hiyo, TBA kama zilivyo taasisi nyingine za Serikali imeweka banda maalum kwa ajili ya kutoa elimu kwa wananchi kuhusu majukumu yake pamoja na kueleza miradi mbalimbali iliyotekelezwa na wakala huo katika kipindi hicho.

Akitembelea mabanda ya taasisi mbalimbali katika viwanja hivyo leo Machi 5, 2026, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule, ameipongeza TBA kwa kutekeleza miradi mikubwa ya Serikali katika mkoa wa Dodoma, ikiwemo ujenzi wa Mji wa Serikali Mtumba pamoja na mradi wa ujenzi wa nyumba 3,500 za makazi ya watumishi wa umma katika eneo la Nzuguni.

Kwa upande wao, wananchi waliotembelea banda la TBA wamepongeza utekelezaji wa mradi wa nyumba za makazi katika eneo la Nzuguni, wakisema umechangia kusogeza huduma za kijamii na biashara karibu na wananchi pamoja na kuimarisha hali ya ulinzi na usalama katika eneo hilo.

 

 

Na Mwandishi Wetu, Handeni

Wanawake katika Halmashauri ya Mji Handeni wametakiwa kutumia simu janja na teknolojia ya kidijitali kwa kuwa ni nyenzo muhimu ya kukuza biashara na kujikwamua kiuchumi kupitia fursa mbalimbali zinazopatikana mtandaoni.

 Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese ameyasema hayo wakati akizindua Jukwaa la Uwezeshaji Wanawake Kiuchumi katika kongamano la wanawake lililofanyika mjini Handeni.

Amesema matumizi sahihi ya simu janja yanaweza kuwasaidia wanawake kupanua masoko ya biashara zao kupitia mitandao ya kijamii pamoja na kupata taarifa muhimu za fursa za kiuchumi zinazotolewa na serikali.

Nyamwese amesema jukwaa hilo limekuja wakati muafaka kutokana na juhudi za serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan katika kuwawezesha kiuchumi wanawake na wasichana.

“Jukwaa hili litawawezesha kupata fursa na kujadiliana namna ya kujikwamua. Mtapata mbinu mbalimbali za kuongeza thamani ya biashara zenu na namna ya kuzifikia fursa zinazotolewa na serikali ikiwamo mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na halmashauri,” amesema.

Aidha, amewasisitiza wanawake kuwa wabunifu katika biashara zao na kutumia kikamilifu teknolojia pamoja na mikopo inayotolewa na halmashauri ili kujiongezea kipato.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Handeni, Maryam Ukwaju amesema halmashauri imeandaa mkakati wa kusaidia vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu kujiunga kwenye mfumo wa ununuzi wa umma wa NeST ili viweze kunufaika na fursa ya asilimia 30 ya zabuni zinazotolewa kwa makundi hayo.

Amesema kupitia mfumo huo vikundi vitapata nafasi ya kushiriki kikamilifu katika zabuni zinazotangazwa na halmashauri na hivyo kuongeza kipato na kukuza uchumi wao.

Akizungumza kuhusu kongamano hilo, Mkurugenzi huyo amesema katika kongamano hilo wanawake walipata elimu mbalimbali ikiwamo masuala ya fedha, msaada wa kisheria, umiliki wa ardhi pamoja na masuala ya ndoa ili kuwajengea uelewa na kuwasaidia kuwa chachu ya maendeleo ya Handeni.

Aliongeza kuwa elimu hiyo pia inalenga kuwawezesha wanawake kushiriki kikamilifu katika kufikia malengo ya maendeleo ya Taifa yaliyowekwa katika Dira ya Maendeleo ya mwaka 2050.

Akisoma taarifa ya uendeshaji wa shughuli za majukwaa ya uwezeshaji wananchi kiuchumi, Mratibu wa majukwaa hayo, Carin Umwambe amesema jukwaa hilo linalenga kuwaunganisha wanawake wajasiriamali na watoa huduma katika sekta za umma na binafsi ili waweze kupata fursa mbalimbali za kiuchumi na kibiashara.

Balozi wa Switzerland nchini Tanzania, Nicole Providoli akishirikiana na viongozi mbalimbali wa Kampuni ya Sika Tanzania wakikata Utepe kuashiria usheherekeaji wa miaka 10 ya kampuni hiyo pamoja na uzinduzi wa mitambo mipya ya kisasa katika miji ya Dar es Salaam na Mwanza. 


KAMPUNI ya kimataifa ya uzalishaji wa kemikali maalum za ujenzi, Sika Tanzania, imeadhimisha miaka 10 ya uwepo wake nchini kwa kuzindua mitambo mipya ya kisasa katika miji ya Dar es Salaam na Mwanza. Hatua hiyo inalenga kuimarisha uzalishaji wa ndani, kuongeza ajira na kuchochea maendeleo endelevu katika sekta ya ujenzi.

Akizungumza katika hafla ya maadhimisho hayo, Meneja Mkuu wa kampuni hiyo, Dennis Ott, alisema uwekezaji huo unaashiria hatua mpya ya ukuaji wa viwanda na ubunifu nchini. Alieleza kuwa upanuzi wa kiwanda cha Dar es Salaam utaongeza uwezo wa uzalishaji na ufanisi wa shughuli za kampuni.

Ott aliongeza kuwa kiwanda kipya cha Mwanza kimejengwa kimkakati ili kuhudumia Kanda ya Ziwa na maeneo ya Magharibi mwa Tanzania, hatua itakayorahisisha upatikanaji wa bidhaa za ujenzi na kuimarisha usambazaji wake katika maeneo hayo.

Kwa mujibu wa kampuni hiyo, uwekezaji huo utaongeza uzalishaji wa ndani, kupunguza utegemezi wa bidhaa zinazoagizwa kutoka nje na kufungua nafasi mpya za ajira katika sekta za uzalishaji na teknolojia za ujenzi.

Katika kipindi cha miaka 10 iliyopita, Sika Tanzania imechangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya sekta ya ujenzi nchini kupitia teknolojia za kuunganisha, kuziba na kuzuia maji pamoja na suluhisho za kisasa za zege zinazotumika katika miradi mikubwa ya miundombinu.

Kupitia programu ya mafunzo ya Sika Academy, kampuni hiyo imefanikiwa kufundisha zaidi ya mafundi na wakandarasi 5,000 wa ndani, hatua iliyosaidia kuimarisha ujuzi wa wataalamu wa sekta ya ujenzi nchini.

Aidha, kampuni hiyo imeshiriki katika zaidi ya miradi 100 mikubwa ya miundombinu na biashara nchini, ikiwemo Julius Nyerere Hydropower Project, Standard Gauge Railway na Kijazi Interchange.

Wakati huo huo, Balozi wa Switzerland nchini Tanzania, Nicole Providoli, amesema Serikali ya Tanzania inaendelea kuunganisha nguvu za wadau mbalimbali kulinda mazingira na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi. Amesisitiza umuhimu wa kuendeleza sera na mikakati ya nishati safi, uhifadhi wa rasilimali za asili na matumizi ya teknolojia rafiki kwa mazingira ili kulinda ustawi wa kizazi cha sasa na kijacho.

Kwa upande wake, Meneja wa Usalama Mahali pa Kazi wa Sika Tanzania, Doto Damian, ambaye pia ni mshindi wa tuzo ya usalama mahali pa kazi, amesema kutambuliwa kwake kupitia tuzo hiyo ni motisha kubwa katika kuendelea kuhimiza utamaduni wa usalama kazini. Amesema mafanikio hayo yanatokana na juhudi za pamoja za wafanyakazi na uongozi wa kampuni katika kuhakikisha mazingira ya kazi yanakuwa salama na yenye tija.

Aidha, Damian amesema ameendelea kutoa elimu kwa mafundi na wadau wa sekta ya ujenzi kuhusu matumizi ya teknolojia ya Kiswisi katika ujenzi wa madaraja hapa nchini. Ameeleza kuwa teknolojia hiyo inasaidia kuongeza ubora, uimara na usalama wa miundombinu ya madaraja, huku akisisitiza umuhimu wa kuzingatia kanuni za usalama na matumizi sahihi ya vifaa vya kisasa katika miradi ya ujenzi.

Picha ya Pamoja ya Balozi wa Switzerland nchini Tanzania, Nicole Providoli na washindi wa tuzo mbalimbali.
Na Khadija Kalili,Kibaha
WAZIRI wa Wizara ya Ujenzi ambaye pia ni Mhe.Mbunge wa Jimbo la Mkuranga Abdallah Ulega amesema kuwa barabara ya TAMCO Mapinga itakamilika katika msimu ujao wa fedha na kuwataka wananchi waendelee kuwa wastahmilivu na adha wanayoipitia sasa.

Waziri Ulega amesema hayo katika kikao cha siku moja cha Bodi ya Barabara ya Mkoa wa Pwani(RRB/CR/01/2025/2026) kilichofanyika tarehe 4 Machi 2026 kwenye Ukumbi wa Mikutano uliopo katika jengo la Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani.

Barabara hiyo inayotoka TAMCO Kibaha hadi Mapinga ambayo pia inaunganisha Mkoa wa Pwani na Dar es Salaam kuwa ni muhimu sana iweze kukamilika katika kukuza uchumi na kurahisisha kazi za kila siku kwa jamii nzima.

Aidha amezitaja barabara zingine ambazo ziko katika mpango mkakati wa ujenzi kuwa ni Bagamoyo kwenda Mlandizi,Makofia hadi Mzenga na barabara ya Kibaha hadi Kiluvya pamoja na barabara zingine muhimu huku lengo likiwa kuunganisha Mkoa .

Waziri Ulega amesema kuwa atahakikisha barabara hizo anaziwekea fedha na zipate wakandarasi ili zianze kujengwa huku akisema atatoa kipaumbele kwa miradi mikubwa ya kimkakati yenye sura ya Kitaifa ukiwemo ujenzi wa barabara ya Kibaha ambayo kwa hatua ya awali itajengwa Kilomita 3.6 ambapo kukamilika kwake kutatoa sura nzuri na muonekano uliobora kwa Manispaa ya Kibaha ambayo ndiyo lango kwa Mikoa yote na nchi jirani.

Wakati huohuo Mbunge wa viti Maalum Kibaha Vijijini Mhe.Hawa Mchafu amesema kuwa barabara ya Kongowe - Soga inayoelekea katika Kituo cha Reli ya Mwendokasi( SGR) imekuwa ni kero na changamoto kubwa kwa wananchi wanaotumia barabara hiyo ya vumbi na kero umbali mrefu pia huwa mwiba zaidi hasa katika kipindi cha mvua.

"Tunaomba hii barabara ili iweze kukamillika ichukuliwe na TANROADS nasema hivi kwa sababu TARURA wamekua wakisuasua na kushindwa kwenda na kasi ya maendeleo ambayo wananchi wanatarajia.

Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Richard Muyungi (kulia) akizungumza jambo wakati wa kikao chake na wawakilishi wa Ubalozi wa Uingereza nchini Tanzania uliongozwa na Kiongozi wa Programu Endelevu ya Mazingira kutoka Ubalozi wa Uingereza Nchini Tanzania, Bw. Euan Davidson. Kikao hicho kilifanyika katika Ofisi ndogo ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Luthuli Jijini Dar es Salaam leo Alhamisi Machi 05, 2026.

*****************

Serikali imesema itaendelea kushirikiana na wadau wa maendeleo ili kuhakikisha vipaumbele vya Ajenda ya Mazingira na Mabadiliko ya Tabianchi vinapewa msukumo katika majukwaa ya Kitaifa na Kimataifa.

Hayo yamesemwa leo Jijini Dar es Salaam na Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Dkt. Richard Muyungi wakati wa mazungumzo baina yake naKiongozi wa Programu Endelevu ya Mazingira kutoka Ubalozi wa Uingereza nchini Tanzania, Bw. Euan Davidson.

Dkt. Muyungi amesema Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Rais Dkt. Rais Dkt, Samia Suluhu Hassan imeweka mikakati na mipango mahsusi ya kitaifa kuhusu masuala ya mazingira na tabianchi ambayo inahitaji msukumo na ushirikiano wa karibu na wadau wa maendeleo.

Ameitaja mikakati hiyo ni pamoja na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 ambapo nguzo ya tatu inaelezea kuhusu masuala ya uhifadhi wa mazingira na ustahimilivu dhidi ya mabadiliko ya tabianchi, juhudi zinazolenga kuiwezesha Tanzania kufikia nchi ya kipato cha kati ngazi ya juu ifikapo 2050.

Aidha Dkt. Muyungi amesema kipaumbele kingine kilichopewa msukumo ni pamoja na biashara ya kaboni, ambapo Serikali imeweka mazingira wezeshi kwa wadau na kwakuandaa utaratibu wa kitaifa na kimataifa kwa kuanzisha Kituo cha Taifa cha Kufuatilia Kaboni (NCMC).

“Tanzania tayari ina kanuni na miongozo ya biashara ya kaboni na Kituo cha NCMCtayari kimeanza kazi kikiwa na bodi ya wakurugenzi na kamati ya wataalamu ya uchambuzi wa miradi ya kaboni” asema Dkt. Muyungi.

Dkt. Muyungi ametaja kipaumbele kingine cha Serikali kupitia hifadhi ya mazingira ni pamoja na mkakati wa kuhamasisha jamii kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia ambapo kinara wa kampeni hiyo kitaifa na kimataifa ni Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muunganio wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Akifafanua zaidi, Dkt. Muyungi ameeleza kuwa Tanzania pia inaendelea na utekelezajina Mchango wa tatu wa kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi (NDC 3) ambao umeandaliwa kwa ajili ya kupunguza uzalishaji wa gesi joto na kujenga ustahimilivu wa mazingira.

Kwa upande wake, Kiongozi wa Programu Endelevu ya Mazingira kutoka Ubalozi wa Uingereza Nchini Tanzania, Bw. Euan Davidson amesema Ubalozi huo upo tayari kushirikiana na Ofisi ya Makamu wa Rais ili kufanikisha ajenda ya mazingira na mabadiliko ya tabianchi.

“Tupo tayari kushirikiana na Ofisi ya Makamu wa Rais katika masuala ya Uchumi wa Buluu, biashara ya kaboni, teknolojia ya nishati safi ya kupikia na ukamilishwaji wa mchango wa taifa wa kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi” amesema Bw. Davidson.
Kiongozi wa Programu Endelevu ya Mazingira kutoka Ubalozi wa Uingereza nchini Tanzania, Bw. Euan Davidson (kushoto) akizungumza jambo na Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Dkt. Richard Muyungi wakati wa mazungumzo baina yao yaliyofanyika katika Ofisi ndogo ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Luthuli Jijini Dar es Salaam leo Alhamisi Machi 05, 2026.
Mshauri wa masuala ya mazingira kutoka Ubalozi wa Uingereza Bw. Abdallah Shaha(kulia) akizungumza jambo wakati wa kikao baina ya Ubalozi huo na Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Richard Muyungi kilichofanyika katika Ofisi ndogo za Ofisi ya Makamu wa Rais, Luthuli Jijini Dar es Salaam leo Alhamisi Machi 05, 2026.
`
Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Richard Muyungi akizungumza jambo wakati kikao chake na wawakilishi wa Ubalozi wa Uingereza uliongozwa Kiongozi wa Programu Endelevu ya Mazingira kutoka Ubalozi wa Uingereza Nchini Tanzania, Bw. Euan Davidson. Kikao hicho kilifanyika katika Ofisi ndogo ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Luthuli Jijini Dar es Salaam leo Alhamisi Machi 05, 2026.


Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Richard Muyungi akiwa katika picha ya pamoja na Kiongozi wa wa Programu Endelevu ya Mazingira kutoka Ubalozi wa Uingereza nchini Tanzania, Bw. Euan Davidson muda mfupi baada ya kumalizika kwa mazunngumzo baina yao yaliyofanyika katika Ofisi ndogo za Ofisi ya Makamu wa Rais, Luthuli Jijini Dar es Salaam leo Alhamizi Machi 05, 2026.

Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Richard Muyungi akiwa katika picha ya pamoja na wawakilishi wa Ubaloziw a Uingereza nchini Tanzania muda mfupi baada ya kumalizika kwa mazunngumzo baina yao yaliyofanyika katika Ofisi ndogo za Ofisi ya Makamu wa Rais, Luthuli Jijini Dar es Salaam leo Alhamizi Machi 05, 2026.

(NA MPIGAPICHA WETU)
Mkutano Maalumu wa 59 wa Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) umefanyika leo tarehe 5 Machi 2026 jijini Arusha, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya mwisho ya Mkutano wa 25 wa Wakuu wa Nchi wanachama wa Jumuiya hiyo utakaofanyika tarehe 7 Machi 2026.

Mkutano huo ambao umepokea na kujadili taarifa ya kikao cha Makatibu Wakuu, pamoja na masuala mengine umekamilisha maandalizi ya ajenda zitakazojadiliwa na kutolewa maamuzi pamoja na maelekezo na Mkutano wa Wakuu wa Nchi wa EAC, ambao ndio chombo cha juu cha maamuzi ndani ya Jumuiya hiyo.

Akizungumza katika ufunguzi wa mkutano huo Mhe. Beatrice Askul Moe Waziri anayesimamia masuala ya Afrika Mashariki Kenya na Mwenyekiti wa Mkutano huo ameeleza kuwa ajenda zilizoandaliwa zitatoa mwelekeo mpya wa utatuzi wa changamoto mbalimbali zinazoikabili Jumuiya kwa sasa ikiwemo uhaba wa rasilimali fedha za kuendesha shughuli mbalimbali za Sekretariati ya EAC na upungufu wa wafanyakazi.

Aidha, ametoa rai kwa wajumbe wa mkutano huo kuendelea kuimarisha na kudumisha ushirikiano uliopo katika Jumuiya, huku akibainisha kuwa kutokana na ushirikiano huo umeziwezesha nchi Wanachama kuweza kuhimili misukosuko inayosababishwa na kuyumba kwa uchumi wa dunia ikiwemo ongezeko la bei za bidhaa muhimu kama vile chakula.

Miongoni mwa ajenda muhimu zinazotarajiwa kuwasilishwa na kujadiliwa katika mkutano huo wa 25 wa Wakuu wa Nchi ni pamoja na maendeleo ya utekelezaji wa Itifaki ya Soko la Pamoja la EAC, kuondolewa kwa vikwazo visivyo vya ushuru (Non-Tariff Barriers – NTBs), kukubaliana kuhusu kanuni ya uchangiaji wa michango ya Jumuiya, pamoja na kuimarisha ushirikiano katika sekta za utalii, miundombinu na nishati.

Kwa sasa, Jumuiya ya Afrika Mashariki inaundwa na nchi wanachama nane ambazo ni Tanzania, Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi, Sudan Kusini, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) na Somalia, ikiwa na jumla ya idadi ya watu inayokadiriwa kufikia zaidi ya milioni 300 na pato la pamoja la uchumi (GDP) linalokadiriwa kuzidi dola za Marekani bilioni 300.

Ujumbe wa Tanzania katika mkutano huo umeongozwa na Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb), Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, ukijumuisha Naibu Mawaziri kutoka sekta mbalimbali wakiwemo; Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde Naibu Waziri Fedha, Mhe. Regina Ndege Qwaray, Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora na Mhe. Dennis Lazaro Londo Naibu Waziri Viwanda na Biashara na Viongozi wengine Waandamizi wa Serikali.













Mkuu wa Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT), Dkt. Prosper Mgaya, amesema kuna umuhimu mkubwa wa kuongeza ushiriki wa watoto wa kike katika masomo ya sayansi na uhandisi ili kuwapa fursa sawa katika taaluma hizo muhimu kwa maendeleo ya nchi.

Dkt. Mgaya ameyasema hayo wakati wa ziara ya wanafunzi wa Shule ya Sekondari Tuliani iliyopo Magomeni walipotembelea chuoni hapo kwa lengo la kujifunza na kujionea mazingira halisi ya masomo ya sayansi na uhandisi yanavyotolewa.

Amesema chuo hicho kwa kushirikiana na Benki ya Dunia kinaendelea kutekeleza mradi wa kuanzisha Kituo cha Umahiri cha masuala ya usafiri wa anga, ambacho kitakuwa na majengo pamoja na vifaa vya kisasa vinavyofanana na vile vinavyopatikana katika vyuo vikuu vya kimataifa.

Kwa mujibu wa Dkt. Mgaya, ziara ya wanafunzi hao imelenga kuwapa fursa ya kuona kwa vitendo mazingira ya kujifunzia pamoja na vifaa vinavyotumika katika taaluma za urubani na matengenezo ya ndege, ili kuwasaidia kupata mwamko na uelewa kuhusu fursa zilizopo nchini katika masomo ya sayansi na uhandisi.

Amefafanua kuwa takwimu zinaonesha ushiriki wa watoto wa kike katika kozi za sayansi na uhandisi bado ni mdogo, ambapo kwa sasa hauzidi asilimia 15, licha ya uwezo mkubwa wanafunzi wa kike wanaouonesha wanapopata nafasi ya kusoma masomo hayo.

Ameongeza kuwa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imekuwa ikiendesha programu mbalimbali za kuhamasisha watoto wa kike kujikita katika masomo ya sayansi, huku NIT pia ikiendelea kutembelea shule mbalimbali nchini kutoa uelewa kuhusu fursa za masomo hayo.

Kwa upande wake, Mkuu wa Shule ya Sekondari Tuliani, Happiness Mailo, amesema ziara hiyo imekuwa na manufaa makubwa kwa wanafunzi, hasa wa kike, kwa kuwa imewapa fursa ya kuona kwa vitendo mazingira ya masomo ya sayansi na uhandisi na hivyo kuwajengea hamasa ya kuyachagua katika masomo yao ya baadaye.

Amesema wanafunzi wengi wa kike hukata tamaa mapema kutokana na dhana potofu kuwa masomo ya sayansi ni magumu, hivyo ziara kama hizo husaidia kubadilisha mtazamo huo na kuwahamasisha kujiamini zaidi katika masomo yao.

Naye mwanafunzi wa kidato cha pili katika Shule ya Sekondari Tuliani, Lissa Ramadhani, amesema ziara hiyo imewasaidia kufahamu zaidi kuhusu taaluma za sayansi na uhandisi ambazo awali waliziona kuwa ngumu au zisizowahusu.

Amehimiza wanafunzi wengine wa kike kuondoa hofu na kujiamini katika kusoma masomo ya sayansi, akisema kuwa fursa za taaluma hizo ni nyingi na zina mchango mkubwa katika maendeleo ya taifa.











Top News