Na Byera Deus

Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) limeanza kulipa fidia kwa wananchi 280 wa kata nne za Wilaya ya Karagwe wanaopitiwa na mradi wa kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 220 kutoka Benaco hadi Kyaka, kufuatia maagizo yaliyotolewa Mei 9, 2026, na Waziri wa Nishati, Deogratias Ndejembi, wakati wa ziara yake mkoani Kagera.

Mhandisi anayehusika na masuala ya kuchora ramani na kupima ardhi katika mradi huo kutoka Makao Makuu ya TANESCO, Derick Kaijanangoma, alisema jumla ya shilingi bilioni 1.7 zimetolewa kwa ajili ya ulipaji fidia katika awamu ya kwanza kwa wananchi wa kata za Nyaishozi, Nyakahanga, Bugene na Nyakasimbi.

Alisema gharama za mradi za kulipa fidia ni shilingi bilioni 6.1, na Serikali imeanza kutoa fedha kwa wananchi wote wanaopisha ujenzi wa mradi huo katika wilaya za Ngara, Karagwe na Missenyi.

“Zoezi la ulipaji fidia tayari limefanyika katika Wilaya ya Ngara na sasa linaendelea katika maeneo ya Karagwe. Tunajua kwamba tathmini ilifanyika mwaka 2022, lakini sasa muda wa kulipwa fidia umefika, na kila familia itafikiwa. Hata kama muhusika amepoteza maisha, kama nyaraka zimetimia na vigezo vimezingatiwa, atapatiwa haki yake,” alisema Kaijanangoma.

Alisema kuwa baada ya kulipwa fidia, wananchi hawataruhusiwa kuendelea kufanya shughuli zozote za kibinadamu katika maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya mradi, na wametakiwa kuondoa mali zao ndani ya siku 30, huku uwezekano wa kuongezewa muda ukiwepo pale inapobidi ili kumpa nafasi mkandarasi kuendelea na kazi.

Alitoa wito kwa wananchi waliopokea fidia kuhakikisha wanarudisha kilekile kilichofidiwa, kama ni ardhi, nyumba au misitu, na wasitumie fedha hizo katika masuala mengine kama kuongeza mke au kukimbia familia.

Sarafina Gasiliel, Afisa Maendeleo ya Jamii wa mradi huo, alisema changamoto kubwa ambazo wamekutana nazo katika ulipaji wa fidia ni migogoro ya ndoa, migogoro ya ardhi ambayo tayari imethaminishwa pamoja na ukosefu wa elimu ya mirathi.

Alitoa wito kwa wananchi kumaliza migogoro kwanza ili fidia ijulikane inaenda kwa nani, huku wananchi wote waliopoteza ndugu zao waliopaswa kulipwa fidia wakitakiwa kupata msimamizi wa mirathi atakayeweza kupokea fidia hiyo kwa niaba ya wanafamilia wa marehemu.

Kwa upande wao, baadhi ya wananchi akiwemo mkazi wa Kijiji cha Bisheshe, Fidelix Banyesige, wameishukuru Serikali na TANESCO kwa kuanza kulipa fidia licha ya kuchelewa kwake tangu walipofanyiwa tathmini mwaka 2022.

“Tunalishukuru shirika kwa kutulipa fidia. Ingawa imechelewa, tuko tayari kupisha mradi huu kwa manufaa ya wananchi wengine ambao bado hawajapata huduma ya umeme,” alisema Banyesige kwa niaba ya wananchi hao.

Mradi huo wa kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 220 unatarajiwa kuboresha upatikanaji wa huduma ya umeme katika maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Kagera na kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii.









Na Said Mwishehe,Michuzi TV 

DIWANI wa Kata Kariakoo Haji Manara ametoa ombi malaamu kwa Baraza la Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam pamoja na Mkurugenzi wa Jiji hilo kuja na ajenda maalum ya kuhakikisha Dar es Salaam inakuwa safi kuelekea michuano ya AFCON.

Tanzania na hasa Jiji la Dar es Salaam imepewa heshima ya kuwa mwenyeji wa ufunguzi wa michuano ya AFCON hivyo matarajio kutakuwa na maelfu ya wageni kutoka mataifa mbalimbali,hivyo kuwa na ajenda ya kudumu kwa ajili ya kuliboresha Jiji hilo ni muhimu ikawa ya kudumu kuanzia sasa.

Akiwasilisha maombi maalum katika Kikao cha Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam kilichofanyika leo Mei 14,2026 ,Manara ametumia nafasi hiyo kuzungumzia hatua zinazopaswa kuchukuliwa na Mkurugenzi wa Jiji na Meya kuhakikisha Jiji linakuwa safi.

“Mungu akitujaalia mwakani Tanzania  itakuwa mwenyeji michuano ya AFCON na ufunguzi utanyika jijini Dar es Salaam na kutakuwa na mechi zitakzochezwa Dar es Salaam.Hivyo naomba tuwe na ajenda ya kudumu itakayokuwa inajadili kwa kushirikiana na kamati ya maandilizi na serikali yetu

“Sura ya Dar es Salaam inaendelea kupendeza lakin lazima tufanye jitihada za kuhakikisha Jiji linakuwa safi kwani itakuwa aibu kuwa na Jiji  chafu,mitaro kujaa maji, lakini kuwa na misongamano isiyokuwa na ulazima.

“Pia kuelekea AFCON lazima tuandae watu wa kupokea wageni,hivyo Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Sslaam nakuomba ubebe ajenda hii.Jiji la Dar es Salaam kuna Hoteli zenye hadhi ya Five Star tano ambazo zinaweza kupokea maelfu ya wageni.”

Akifafanua zaidi Manara amesema pamoja na uwepo wa hoteli hizo iko haja kwa Mkurugenzi pamoja na Meya kuangalia uwezekano wa kuzungumza na wamiliki wa Apatiment ili ziweze kupokea wageni kwani wapo watakaotoka mikoani ambapo sio wote wanaweza kufikia kwenye hoteli kubwa,hivyo watafikia kwenye apatimenti ziliozopo.

“Naomba tuzungumze na wamiliki wa Apatiment kwa ajili ya kupokea wageni,kwani sio watu wote ambao wataweza kukaa Hayat Regency na hoteli nyingine kubwa za namna hiyo, hivyo wengine watakaokuja watakaa huko,”amesema Manara.

Wakati huo huo amesema kwa upande mwingine Jiji la Dar es Salaam limekuwa nyuma katika utalii hivyo iko haja ya kuwa na kumbi maalum ambazo zitakuwa zinatumika katika utalii katika kipindi ambacho michuano ya AFCON itakuwa inaendelea.







Na Said Mwishehe,Michuzi TV

MEYA wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam Nurdin Bilali maarufu Shetta amesema anatambua na kupongeza kazi nzuri inayofanywa na Baraza la madiwani pamoja na watumishi wote wa halmashauri hiyo.

Aidha amesema kutokana na ushirikiano baina ya viongozi wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam ni wazi wataendelea kutekeleza majukumu yao na kubwa zaidi ni kuifanya halmashauri hiyo kuwa namba moja nchini katika kukusanya mapato.

Akizungumza katika kikao cha Baraza la Mdiwani Robo 3 ya mwaka 2026 kuanzia Januari hadi Machi katika Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam kilichokutana kujadili taarifa za utendaji kazi wa kata za Halnashauri ya Jiji la Dar es Salaam.

“Naomba kutambua kazi nzuri inayofanywa na kila mmoja wetu katika halmashauri yatu na viongozi wa kitaifa wamekuwa wakipongeza baraza letu kwa kazi nzuri inayofanyika,ukweli tunapokea sifa nyingi.

“Tuendelee kuwa halmashari namba moja katika kukusanya mapato,kufanya kazi kwa bidii na hatimaye kuilete heshima nchi yetu pamoja na kumletea heshima Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Rais Dk.Samia Suluhu Hassan.

Katika kikao hicho pia Baraza la Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam limeshuhudia Diwani Mteule wa Viti Maalum Gema Ishengoma akila kiapo cha kuwa Diwani ambapo Meya Bilal ametumia nafasi hiyo kumkaribisha huku akiomba madiwani na watumishi wa Jiji hilo kumpatia ushirikiano ili aweze kutimiza majukumu yake kwa maendeleo ya wananchi.

“Chama Cha Mapinduzi(CCM)kama kilivyokuwa ltanuru la kupika viongozi kuanzia jumuiya ya chipukizi basi hata diwani aliyekuja atatusaidia katika baraza la halmashauri na kubwa zaidi tutampa ushirikiano ili apate nafasi ya kufanya kazi vizuri








-DCEA kuja na operesheni maalum kuwabaini, vijana walioko vyuo vikuu,katika vijiwe waonywa



Na Said Mwishehe,Michuzi TV

MAMLAKA ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya(DCEA) imetoa onyo kwa watumishi wa Serikali wanaojihusisha na dawa za kulevya au wanatumia itawachukulia hatua za kisheria pamoja na kufukuzwa kazi.

Aidha imesema kwa vijana ambao wanaomba ajira serikali kabla ya kuajiriwa Mamlaka hiyo kwa kushirikiana na mamlaka nyingine itahakikisha inawapima na wale wote ambao watabainika wanatumia dawa za kulevya hawatapa ajira serikalini.

Hayo yamesemwa leo Mei 13,2026 jijini Dar es Salaam na Kamishina Jenerali wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya Aretas Lyimo alipokuwa akijibu maswali ya waandishi wa habari baada ya kutoa taarifa ya operesheni iliyofanywa na mamlaka hiyo Aprili mwaka huu.

Katika maswali ya waandishi walitaka kufahamu hatua gani zinachukuliwa na Mamlaka hiyo kukomesha matumizi ya dawa za kulevya hasa katika vijiwe ambavyo vimeonekana kuwa soko la dawa za kulevya hasa mirungi na bangi.

“Tumeanzisha mpango wa kuhakikisha kwamba watumishi wa Serikali wote watakaobainika kwa namna moja au nyingine wanajihusisha na dawa za kulevya au wanatumia tutawachukulia hatua za kisheria na pamoja na kufukuzwa kazi

“Kwenye vyombo vya dola kuna mkakati tayari wanaoingia au kuajiriwa tutawapima kabla hawajaajiriwa ili tunapowabaini wale wanaotumia dawa za kulevya basi ina maana ajira yao imeishia haahpo.

“Nitoe mwito kwa vijana walioko vyuo vikuu ambao wao ndio wanatumia dawa za kulevya zaidi kutokana na mtindo wa maisha pamoja na kuingia kwenye makundi mbalimbali waache.”

Kamishina Jenerali Lyimo amefafanua vijana wakishatumia dawa za kulevya suala la kuajiriwa asahau kwenye vyombo vya dola na kusisitiza kabla ya kupata ajira kwasababu watahakikisha wale waliongia kwenye dawa za kulevya wanawapima kabla hawajaajiriwa.

“Na tumeanza na vyombo vya dola hivyo tutahakikisha tunaenda katika maeneo yote ili kuhakikisha tunakomesha matumizi ya dawa za kulevya ndani ya Serikali lakini nje ya Serikali ili kwa pamoja tujenge jamii imara.

“Jamii yenye kufanya kazi kwa bidii na itakayokuza uchumi wa Tanzania ,tuwe na Tanzania isiyokuwa na matumizi ya dawa za kulevya ,hiyo ndio dhamira ya Serikali.

“Pia tutakwenda kwenye vijiwe ambako ndio soko kuu la kuuza dawa za kulevya tunao mkakati maalum.Tutafanya operesheni kuhakikisha kwamba tunavunja vijiwe vya dawa za kulevya katika maeneo mbalimbali,”amesema Kamishina Jenerali Lyimo.


MSTAHIKI Meya wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Alimwoni Chaula ameeleza kuwa jiji linaendelea kuthamini mchango wa wadau wa maendeleo katika kuimarisha mifumo ya chakula mijini kupitia ushirikiano unaolenga ustawi wa wananchi na maendeleo endelevu.

Akizungumza katika kikao cha wadau kuhusu uanzishwaji wa Jukwaa la Wadau wa Mifumo ya Chakula wa Jiji la Dodoma alianza kwa kuwashukuru watekelezaji wa Mradi wa Tukue kwa Pamoja “Growing Together” unaotekelezwa na IDH kupitia RIKOLTO kwa kuendelea kuwa mshirika muhimu wa Jiji la Dodoma katika safari ya kuimarisha mifumo ya chakula mijini.

“Kwa kutumia nafasi hii, napenda kuwashukuru kwa dhati watekelezaji wa Mradi wa Tukue kwa Pamoja kwa kuendelea kuwa mshirika wa karibu wa Jiji la Dodoma katika safari ya pamoja ya kuimarisha mifumo ya chakula mijini. 

Ushirikiano huu unaweka msingi imara wa kuhakikisha upatikanaji wa chakula salama, chenye lishe na kwa gharama nafuu tukizingatia jiji letu linakuwa kwa kasi. Kwahiyo, mahitaji ya mifumo madhubuti ya chakula lazima iwepo” alisema Chaula.

Aidha, alisema kuwa kutokana na changamoto mbalimbali ikiwemo mabadiliko ya tabianchi, kupanda kwa bei za bidhaa na utegemezi mkubwa wa chakula kutoka nje ya jiji, ipo haja ya kuwa na jukwaa la pamoja litakalowakutanisha wadau mbalimbali kwa ajili ya kupanga na kuratibu mikakati ya kuimarisha usalama wa chakula.

 “Uanzishwaji wa Jukwaa la Wadau wa Mifumo ya Chakula wa Jiji la Dodoma si hiari bali ni hitaji la msingi katika kuhakikisha tunakuwa na mfumo wa chakula ulio imara, jumuishi na endelevu” alisema Chaula.

Katika hatua nyingine, alisisitiza kuwa Jiji la Dodoma linaunga mkono kikamilifu uanzishwaji wa jukwaa hilo na lipo tayari kuhakikisha linaunganishwa katika mipango na mifumo rasmi ya halmashauri ili kuongeza ufanisi wa utekelezaji wa sera zinazohusiana na lishe, afya, biashara na maendeleo ya miji.

Nae, Afisa Lishe Jiji la Dodoma, Semeni Eva Juma alisema kuwa chakula bora kinapaswa kuwa na virutubisho kamili. “Suala la kuwa na mifumo imara ya chakula tunapaswa kulipa kipaumbele kwasababu chakula bora na chenye afya inabidi kiwe katika makundi sita. Tunapongeza mradi huu, unatija kubwa sana katika kuboresha mifumo ya chakula. Tutaendelea kutoa elimu kwa jamii ili kujenga kizazi imara” alisema Juma.

Halmashauri ya Jiji la Dodoma imeonesha kuwa kupitia ushirikiano madhubuti wa wadau mbalimbali, jukwaa hilo litakuwa chachu ya kuimarisha usalama wa chakula, kuongeza ustawi wa wananchi na kujenga mfumo wa chakula wenye uwezo wa kukabiliana na changamoto za sasa na zijazo.





Wanawake wajasiriamali wa Kata ya Ludete sasa watapata nafasi ya kufanya shughuli zao bila wasiwasi, kufuatia uamuzi wa kuanzisha kituo cha kulelea watoto wadogo katika kata hiyo.

Akizungumza na wananchi wa Mtaa wa Afya jana, Diwani wa Kata ya Ludete, Jumanne Misungwi, alisema ujenzi wa kituo hicho unatarajiwa kuanza mwezi Julai mwaka huu.

“Kituo hiki kinalenga kutoa mazingira salama kwa watoto wadogo, ili mama zao waweze kwenda kufanya shughuli za ujasiriamali na kujikwamua kiuchumi,” alisema Misungwi.

Pia aliwaasa wananchi kuendelea kufanya kazi kwa bidii, huku akiahidi kuwa serikali itaendelea kuandaa mazingira wezeshi kwao kujituma na kujiletea maendeleo.

Kwa upande wake, Mtendaji wa Kata ya Ludete, John Katanga, alifafanua kuwa kituo hicho kitahudumia watoto wenye umri wa chini ya miaka mitatu.

“Mpango huu utawapa mama nafasi ya kwenda kazini na kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi bila kuwa na wasiwasi na watoto wao,” alisema Katanga.

Aidha, Diwani Misungwi aliwaomba wazee na wananchi wote waendelee kumuombea ili aweze kutekeleza majukumu aliyopewa na wananchi kwa ufanisi. Pia aliwataka kumuunga mkono ili Kata ya Ludete ipate maendeleo makubwa zaidi.







Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa amesema wizara hiyo inaomba kuidhinishiwa jumla ya Shilingi 433.3 bilioni kwa ajili ya utekelezaji wa majukumu yake katika mwaka wa fedha 2026/2027.

Akiwasilisha hotuba ya makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara hiyo leo Bungeni jijini Dodoma, Waziri Bashiru amesema fedha hizo zitatumika kugharamia matumizi ya kawaida pamoja na miradi mbalimbali ya maendeleo katika sekta ya mifugo na uvuvi.

Kwa mujibu wa Waziri huyo, kati ya fedha zinazoombwa, Shilingi 98.2 bilioni zimetengwa kwa ajili ya matumizi ya kawaida, huku Shilingi 335.1 bilioni zikielekezwa kwenye utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Amefafanua kuwa ndani ya bajeti ya matumizi ya kawaida, Shilingi 49.4 bilioni ni kwa ajili ya mishahara ya watumishi wa wizara hiyo, huku Shilingi 48.8 bilioni zikitengwa kwa matumizi mengineyo ya uendeshaji wa shughuli za kila siku za wizara.

Kwa upande wa fedha za maendeleo, Waziri Bashiru amesema Shilingi 193.7 bilioni zinatarajiwa kutoka katika vyanzo vya ndani, wakati Shilingi 141.3 bilioni zitakuwa fedha za nje kutoka kwa washirika wa maendeleo.

Waziri huyo amesema fedha hizo zitasaidia kuendelea kuimarisha sekta ya mifugo na uvuvi nchini kupitia utekelezaji wa miradi mbalimbali yenye lengo la kuongeza uzalishaji, kuboresha miundombinu, kuendeleza uvuvi wa kisasa pamoja na kuongeza mchango wa sekta hizo katika uchumi wa taifa.

Aidha, alitumia nafasi hiyo kutoa shukrani kwa Spika wa Bunge na wabunge wote kwa kuisikiliza na kuijadili hotuba hiyo, huku akibainisha kuwa hotuba kamili ya bajeti hiyo inapatikana kupitia tovuti rasmi ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi.


Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma .

Shughuli za Bunge jijini Dodoma zilisimama kwa muda leo Alhamisi Mei 14, 2026 baada ya kutokea hitilafu ya mfumo wa sauti ndani ya ukumbi mkuu wa Bunge, hali iliyomlazimu Spika wa Bunge, Mussa Azan Zungu kuahirisha kikao hicho kwa muda.

Tukio hilo limetokea majira ya saa 2:59 asubuhi wakati Spika akiingia ukumbini akiwa ameongozana na timu ya makatibu wa Bunge pamoja na wapambe wa Bunge waliokuwa wakiongozwa na mbeba Siwa. Licha ya vipaza sauti kuonekana kuwaka ukumbi mzima, hakukuwa na sauti yoyote iliyokuwa ikisikika.

Hitilafu hiyo ilianza kubainika mara baada ya sauti ya mpambe anayebeba Siwa kushindwa kusikika wakati akiashiria kuwasili kwa kiongozi wa Bunge, huku akionekana akizungumza bila sauti kufika kwa wabunge na wageni waliokuwapo ukumbini.

Baada ya Spika kusimama tayari kwa ajili ya kusoma dua ya kuanza kikao, sauti yake nayo haikusikika, jambo lililosababisha taharuki ya muda mfupi ndani ya ukumbi huo. Dakika chache baadaye, mmoja wa wapambe aliingia na kuondoa Siwa kutoka sehemu yake ya kawaida kabla ya kuihifadhi kwenye droo ya meza ya mbele.

Muda mfupi baada ya hali hiyo, Spika Zungu aliondoka kwenye kiti chake huku Waziri Mkuu, Mwigulu Nchemba naye akisimama na kuondoka ukumbini.

Baadaye wapambe wa Bunge walionekana wakilibeba Siwa ndani ya sanduku maalumu na kutoka nalo nje ya ukumbi, huku mfumo wa vipaza sauti ukiendelea kuonyesha mwanga wa kuwaka lakini bila kutoa sauti yoyote.

Tukio hilo limejiri siku moja tu baada ya kusikika kwa mlio wa king’ora ndani ya ukumbi wa Bunge uliozua taharuki miongoni mwa wabunge kabla ya Mwenyekiti wa Bunge, Deo Mwanyika kueleza kuwa hakukuwa na hatari yoyote na shughuli za Bunge kuendelea kama kawaida.

Kwa mujibu wa taarifa zilizopatikana ndani ya Bunge, kikao hicho kinatarajiwa kuendelea baadaye katika Ukumbi wa Pius Msekwa wakati mafundi wakiendelea kushughulikia hitilafu iliyojitokeza kwenye mfumo wa sauti wa ukumbi mkuu.



 

Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Mhe. Kanal Donald Msengi, amewashauri Viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuwahimiza wakulima kutumia Mfumo wa Stakabadhi za Ghala ili kuleta mabadiliko chanya kiuchumi na kuongeza tija katika uzalishaji wa mazao.

Akizungumza  wakati wa Mafunzo ya Mfumo wa Stakabadhi za Ghala kwa Viongozi wa Chama na Serikali kutoka mkoa wa Dodoma yaliyofanyika mkoani Mtwara, Kanal Msengi amesema mfumo huo umeleta mafanikio makubwa kwa vyama vya ushirika mkoani humo kwa kuviwezesha kuwa imara kiuchumi. Ameeleza kuwa kupitia mfumo huo, vyama vimefanikiwa kufanya uwekezaji mbalimbali ikiwemo ujenzi wa maghala, ununuzi wa magari, uanzishaji wa viwanda pamoja na kuchangia huduma za kijamii kama elimu, afya na maji.

“Ni muhimu viongozi mkatumia nafasi zenu kuwahamasisha wakulima na wanaushirika kutumia mfumo huu, kwani umeleta manufaa makubwa na una uwezo wa kuleta mageuzi chanya kwa sekta ya kilimo,” amesema Kanal Msengi.

Naye Kaimu Mrajis Msaidizi wa Mkoa wa Mtwara, Robert Nzunza, amebainisha hatua muhimu za mchakato wa stakabadhi za ghala kuwa ni pamoja na maandalizi ya msimu wa mauzo, ukusanyaji wa mazao ghalani, usafirishaji wa mazao kwenda ghala kuu, mapokezi ya mazao, mauzo kupitia minada ya mtandao, malipo ya fedha kupitia vyama vikuu (Unions), malipo kwa wakulima na wadau, pamoja na utoaji wa mizigo ghalani.

Kwa upande wake Mkuu wa msafara huo ambaye pia ni Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa kutoka mkoa wa Dodoma, Donald Mejetii, amesema kuwa mafunzo hayo yatawasaidia kuwajengea uwezo viongozi hao ili waweze kuwahamasisha wakulima wa Dodoma kutumia mfumo huo kwa tija zaidi.

Viongozi wa Chama na Serikali kutoka mkoa wa Dodoma wapo mkoani Mtwara kwa ziara ya kujifunza Mfumo wa Stakabadhi za Ghala katika vyama vya ushirika na namna unavyoweza kuinua kipato cha mkulima. Katika ziara hiyo pia wametembelea Chama Kikuu cha Ushirika cha MAMCU LTD pamoja na Chama cha Msingi Mayanga AMCOS.



Na Janeth Raphael MichuziTv – Dodoma

Mashirika yasiyo ya kiserikali (AZAKI) yameiomba Serikali kupitia Bunge kuhakikisha asilimia tatu ya mapato ya halmashauri nchini zinatengwa mahsusi kwa ajili ya huduma za ulinzi na usalama wa mtoto, hatua inayolenga kuimarisha mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia na malezi yasiyo salama kwa watoto.

Wito huo umetolewa katika warsha ya wabunge kuhusu masuala ya ulinzi wa mtoto iliyoandaliwa na Shirika la World Vision Tanzania, ambapo Kamati za Kudumu za Bunge za PAC, LAAC pamoja na Kamati ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii zilishiriki kupokea mapendekezo kutoka kwa asasi za kiraia ili kuyafikisha bungeni.

Akizungumza katika warsha hiyo, mwakilishi wa asasi za kiraia, Ombeni Kimaro, alisema bado kuna ongezeko la vitendo vya ukatili dhidi ya watoto katika maeneo mbalimbali nchini, hali inayohitaji hatua za haraka za kisera na kifedha ili kukabiliana nayo.

Amesema ipo haja ya Serikali kuhakikisha fedha hizo zinaingizwa katika bajeti za taifa pamoja na halmashauri ili kuwezesha utekelezaji wa mipango ya ulinzi wa mtoto na huduma za kijamii zinazohusiana na ustawi wa watoto.

“Tunataka kuona suala la ulinzi wa mtoto linapewa uzito wa kitaifa. Halmashauri zitenge fedha maalum kusaidia mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia na kuhakikisha watoto wanakuwa katika mazingira salama,” alisema Kimaro.

Aidha, alisema kupungua kwa misaada kutoka kwa wafadhili wa kimataifa kwa mashirika yanayojihusisha na ulinzi wa mtoto kunapaswa kuwa chachu kwa Serikali kuongeza uwekezaji wa ndani katika sekta hiyo muhimu kwa maendeleo ya taifa.

Kwa mujibu wa Kimaro, kutotengwa kwa fedha hizo kunaweza kuchangia kuongezeka kwa changamoto za malezi, maadili na usalama wa watoto pamoja na vijana nchini.

“Bila kufanya hivyo tunaweza kujikuta tunazalisha kizazi kisicho salama na kisicho na maadili. Ulinzi wa mtoto ni uwekezaji wa moja kwa moja kwa taifa la baadaye,” alisisitiza.

Akizungumza kwa niaba ya wabunge, Mwenyekiti wa Kamati ya PAC, Devotha Minja, alisema kamati hiyo ipo tayari kulisemea suala hilo bungeni ili kuhakikisha mapendekezo hayo yanafanyiwa kazi na fedha zinatengwa katika halmashauri zote nchini.

Kwa upande wake, mwakilishi wa Kamati ya LAAC, Josephine Kapone, alisema kamati hiyo itashirikiana na kamati nyingine kuhakikisha suala la ulinzi wa mtoto linapata usimamizi na utekelezaji unaostahili.

Naye mwakilishi wa Kamati ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii, Kafti Kafti, alisema kamati yao itaendelea kufuatilia kwa karibu utekelezaji wa mapendekezo hayo kwa kuwa ndiyo yenye dhamana ya moja kwa moja katika masuala ya ustawi wa mtoto.

Mtafiti na mchambuzi kutoka HakiElimu, Joshua Mwakalikamo, alisema tafiti mbalimbali zimekuwa zikionesha umuhimu wa kuwekeza katika ulinzi wa mtoto ili kujenga jamii salama na yenye maadili bora.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Mipango na Udhibiti Ubora wa World Vision Tanzania, AZAKI ZAITAKA SERIKALI KUTENGA 3% KWA ULINZI WA MTOTO.




Na Mwandishi Wetu, Zimbabwe

Tanzania imeendelea kung’ara katika ukanda wa Kusini mwa Afrika baada ya kutajwa kuwa miongoni mwa nchi zinazoongoza kwa mifumo madhubuti ya usimamizi wa maafa, hatua inayozifanya nchi nyingine wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) kujifunza kupitia uzoefu wake.

Hayo yameelezwa na Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Kaspar Mmuya wakati akimwakilisha Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Mhe. Balamagamba Kabudi wakati wa Mkutano wa Sita wa Kawaida wa Kamati ya Mawaziri Wanaohusika na Usimamizi wa Maafa kwa nchi wanachama wa SADC unaofanyika mjini Masvingo, Zimbabwe.

Amesema Tanzania imefanikiwa kuimarisha mifumo ya kuzuia, kupunguza madhara, kujiandaa na kurejesha hali baada ya maafa kutokana na uwekezaji mkubwa uliofanywa katika sekta ya uratibu wa maafa nchini.

Kwa mujibu wa Mhe. Mmuya amesema moja ya mafanikio makubwa ni kuanzishwa kwa Kituo cha Ufuatiliaji wa Mwenendo wa Majanga na Tahadhari ya Mapema (National Emergency Operation and Communication Center Situation Room), ambacho kinafanya kazi saa 24 kila siku kufuatilia na kuchambua taarifa za majanga.

“Kwa kupitia kituo hiki, Serikali imeweza kupata taarifa za mapema kuhusu majanga yanayoweza kutokea, kufanya uchambuzi wa madhara na kuweka mikakati ya haraka ya kukabiliana nayo,” alisema Mhe Mmuya

Aliongeza kuwa matumizi ya teknolojia ya kisasa katika ukusanyaji na uchambuzi wa takwimu za wakati halisi yamechangia kuongeza ufanisi wa maamuzi na kurahisisha utoaji wa taarifa rasmi kwa wananchi kuhusu namna ya kujiandaa dhidi ya maafa.

“Tunatumia takwimu za sasa na za zamani kutabiri hatari zinazoweza kujitokeza, jambo ambalo linaisaidia Serikali kupanga kwa usahihi hatua za kurejesha hali na kuendelea kulinda maisha ya wananchi,” alisisitiza.

Aidha, aliwaalika wajumbe kutoka nchi wanachama wa SADC kutembelea Tanzania ili kujionea namna mifumo hiyo inavyofanya kazi pamoja na ubunifu unaotumika katika usimamizi wa maafa.

Mkutano huo wa siku nne umezikutanisha nchi 16 wanachama wa SADC pamoja na wataalamu wa kitaifa na mashirika ya kimataifa kujadili utekelezaji wa programu za kikanda za usimamizi wa maafa na namna ya kuimarisha ushirikiano wa kikanda.

Pamoja na mambo mengine, mkutano huo unatarajiwa kuwa jukwaa muhimu kwa mawaziri na washirika wa maendeleo kujadili uwekezaji katika sekta ya usimamizi wa maafa kwa lengo la kujenga ustahimilivu wa kikanda dhidi ya majanga mbalimbali yanayoendelea kujitokeza duniani.






▪️︎ Dkt. Mwigulu asema Serikali imejipanga kujenga jengo lenye hadhi ya kimataifa

▪️︎ Asema Mwanza itaendelea kuwa kitovu muhimu cha shughuli za kiuchumi Kanda ya Ziwa


WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali inaendelea kuchukua hatua kuhakikisha Uwanja wa Ndege wa Mwanza unaboreshwa na kujengwa katika hadhi ya kimataifa ili kuendana na hadhi ya jiji la Mwanza kama kitovu muhimu cha shughuli za kiuchumi Kanda ya Ziwa.

Amesema hayo bungeni jijini Dodoma wakati akitoa kauli ya Serikali kuhusu hoja ya maendeleo ya Uwanja wa Ndege wa Mwanza iliyowasilishwa na Mbunge wa Magu, Mhe. Boniventura Kiswaga, katika mjadala wa bajeti ya Wizara ya Uchukuzi kwenye Kikao cha 28 cha Mkutano wa Tatu wa Bunge la 13, leo Mei 13, 2026.

Waziri Mkuu amesema Serikali inatambua umuhimu wa Uwanja wa Ndege wa Mwanza na imeendelea kufanya jitihada mbalimbali kuhakikisha unakuwa na uwezo wa kuhudumia ndege kubwa pamoja na kukidhi viwango vya kimataifa.

“Zipo jitihada ambazo zimekuwa zikifanyika kuhakikisha kwamba uwanja wa ndege wa Mwanza unaendana na hadhi ya Mwanza kama kitovu cha shughuli za kiuchumi Kanda ya Ziwa,” amesema.

Aidha, Waziri Mkuu amesema Serikali inaendelea na mazungumzo ya kuongeza eneo la uwanja huo ili kuwezesha upanuzi wa njia ya kurukia ndege (runway) pamoja na maboresho mengine muhimu ya miundombinu.

Katika hatua nyingine, Dkt. Mwigulu amesema Serikali imekubaliana kujenga jengo jipya la abiria litakalokuwa na hadhi ya kimataifa na kuendana na mahitaji ya muda mrefu ya uwanja huo.

“Imekuja kukubalika kwamba tujenge jengo ambalo halitahitaji kubomolewa tena baada ya muda mfupi, bali jengo lenye hadhi na viwango vya viwanja vya ndege vya kimataifa,” amesema.

Ameongeza kuwa Serikali itaendelea na mpango huo sambamba na utekelezaji wa miradi mingine ya viwanja vya ndege nchini, huku akisisitiza kuwa dhamira ya kuifanya Mwanza kuwa kitovu kikubwa cha uchumi kupitia usafiri wa anga ipo pale pale.

Waziri Mkuu amesema Serikali itafanya kikao maalumu na wabunge wa Mkoa wa Mwanza pamoja na wizara husika ili kuondoa changamoto zilizokuwa zikikwamisha utekelezaji wa mradi huo na kuruhusu hatua zinazofuata kuendelea.


Na Seif Mangwangi, Michuzi TV Arusha

BENKI ya CRDB imetangaza neema kwa wanahisa kwa ongezeko la asilimia 38 kutoka sh.65 ya mwaka jana hadi kufikia sh.90 kwa hisa moja mwaka huu 2026.

Akizungumza na waandishi wa habari kuelekea mkutano mkuu wa 31 wa wanahisa Leo Mei16, 2026 Jijini hapa Mwenyekiti wa bodi ya wakurugenzi wa benki ya CRDB Prof. Neema Mori amesema wanahisa wana mchango mkubwa na ni nguzo ya msingi katika maendeleo endelevu.

Aidha amewakaribisha wanahisa kuhudhuria kwa wingi katika semina na mkutano mkuu wa 31 ili kujifunza, kuweka mikakati ya pamoja, kutambua fursa zilizopo, kukaribisha wanahisa wapya na kufahamishwa fursa mpya.

Profesa Neema amesema katika semina watakayoifanya vijana ndio watapewa kipaumbele huku akisisitiza kuwa vijana ndio nguvu ya uwekezaji katika taifa lolote duniani.

"Kupitia semina hiyo vijana wameandaliwa fursa mpya ya uwezeshwaji katika uwekezaji kuhakikisha wanamiliki uchumi mzuri, Mkutano huu ni muhimu sana kwetu, wadau, wanachama na wanahisa kwa ujumla, " amesema.

Amesema kutakuwa na mada 12 za msingi ambazo zitawafanya kufikia mafanikio ya pamoja na kuwataka wanahisa kuendelea kuiamini benki ya CRDB kwa sababu inazingatia misingi na kanuni.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa benki ya CRDB Dkt. Abdulmajid Nsekela amesema benki hiyo imeendelea kuwa imara na kufanikiwa kuvuna faida ya shilingi bilioni 206 kwa kipindi cha mwaka mmoja.

Hata hivyo ameongeza kuwa, ubunifu umeongezeka, na huduma nyingi kwa sasa zinapatikana nje ya benki.

"Mafanikio ya miaka 30 ijayo yanategemea uwekezaji wa kina kwa vijana wa sasa, tutahakikisha tunakuwa nao karibu ili kuandaa wawekezaji wazuri wa kesho. 

Benki yetu imevuka mipaka na imeendelea kufanya vizuri kimataifa, nawashukiru sana wateja wetu kutuamini na kuwekeza kwetu, Kama kampuni inayomilikiwa kwa mfumo wa hisa, wanahisa wana nafasi ya kupata taarifa, kutoa maoni na kufahamu mustakabali wa benki yao, Wito wangu kwenu vijana changamkieni fulsa ambazo benki yenu imewaletea ili kesho muwe wawekezaji wakuu wa CRDB" amesema Dkt. Nsekela.






Top News