Britam Insurance Limited (Tanzania) imewekeza TZS milioni 40 katika mradi wa maji safi unaolenga shule mbili za msingi jijini Dar es Salaam, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha miundombinu inayokabiliana na mabadiliko ya tabianchi pamoja na kuboresha upatikanaji wa maji salama katika taasisi za umma.

Mradi huo, uliotekelezwa kwa ushirikiano na kampuni ya uhandisi ya Davis & Shirtliff, umehusisha ufungaji wa mifumo ya pampu za maji zinazotumia nishati ya sola katika Shule ya Msingi Uhuru Mchanganyiko iliyopo Ilala na Shule ya Msingi Mshikamano iliyopo Kivule. Kama sehemu ya juhudi za utunzaji wa mazingira, shughuli za upandaji miti pia zilifanyika katika Shule ya Msingi Mshikamano ili kusaidia uhifadhi wa mazingira.

Mtendaji Mkuu wa Britam Tanzania, Farai Dogo, alisema kuwa “mradi huu umebuniwa kushughulikia changamoto za kijamii na kimazingira, huku ukipunguza utegemezi wa umeme katika maeneo yenye changamoto ya upatikanaji wa umeme kwa uhakika.”

Meneja wa Masoko wa Britam, Leoncia Makubo, alisema mifumo hiyo ilikamilika baada ya kufanyika utafikia wa mahitaji mwezi Mei 2025, iliyochunguza changamoto za upatikanaji wa maji katika shule mbalimbali kabla ya kuchagua shule hizo mbili kunufaika na mradi huo.

“Uwekezaji huu unaakisi mkakati wetu wa kuwezesha jamii kupitia suluhisho endelevu zinazosaidia pia kulinda mazingira,” alisema Dogo wakati wa uzinduzi wa mradi huo.

Kwa mujibu wa kampuni hiyo, mifumo ya maji inayotumia nishati ya sola inatarajiwa kunufaisha zaidi ya watu 10,000, wakiwemo wanafunzi, walimu, pamoja na jamii inayozunguka shule hizo kwa kuboresha upatikanaji wa maji safi na salama.

Katika Shule ya Msingi Mshikamano, mradi huo unatarajiwa kusaidia shughuli za kila siku za shule ikiwemo maandalizi ya chakula kwa wanafunzi wa awali, sambamba na kuboresha hali ya usafi na mazingira ya afya. Zoezi la upandaji miti lililofanyika shuleni hapo pia linaongeza uelewa wa utunzaji wa mazingira kwa wanafunzi na kusaidia juhudi za uendelevu wa muda mrefu.

Katika Shule ya Msingi Uhuru Mchanganyiko, viongozi wa mradi walieleza kuwa mradi huo utasaidia kuimarisha mazingira jumuishi ya elimu, ikiwemo kuboresha mazingira kwa wanafunzi wenye mahitaji maalum.

Dogo aliongeza kuwa “matumizi ya teknolojia ya pampu za maji zinazotumia nishati ya sola yatasaidia kupunguza utoaji wa hewa ya ukaa pamoja na gharama za uendeshaji ukilinganisha na mifumo inayotumia dizeli au umeme wa gridi, jambo linaloendana na malengo mapana ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.”

Mradi huu ni sehemu ya mpango mpana wa uwajibikaji kwa jamii wa Britam. Kati ya mwaka 2024 na 2025, Britam imesaidia zaidi ya shule 70 kupata huduma bora za maji, imechangia upandaji wa zaidi ya miti 95,000, na kuwafikia zaidi ya watu 90,000 Afrika Mashariki kupitia miradi ya maji, elimu na mazingira.

Kampuni hiyo pia inalenga kupanda miti milioni 6 nchini Tanzania ifikapo mwaka 2030 kama sehemu ya lengo la Britam Group la kupanda miti milioni 60 katika ukanda wa Afrika Mashariki na nchi nyingine ambako kampuni hiyo inaendesha shughuli zake.

Davis & Shirtliff, waliotoa na kufunga mifumo hiyo ya pampu za maji, walisema mifumo hiyo imeundwa kwa ubora wa kudumu kwa muda mrefu na kuhitaji matengenezo madogo, hasa katika maeneo yasiyo na umeme wa uhakika.

Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma 

Waziri wa Afya, Omary Mchenjgerwa amesema Serikali imeendelea kuimarisha mapambano dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza kwa kuongeza huduma za matibabu, kinga na elimu kwa jamii, hatua iliyochangia kuongezeka kwa kliniki za kisukari na shinikizo la damu nchini.

Akizungumza leo Mei 11, 2026 bungeni jijini Dodoma wakati akiwasilisha hotuba ya makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Afya kwa mwaka wa fedha 2026/2027, Mchenjgerwa amesema wizara imeendelea kuimarisha uratibu na utekelezaji wa afua za magonjwa ya kisukari, shinikizo la damu pamoja na magonjwa sugu ya mfumo wa upumuaji.

Amesema katika kipindi cha Julai 2025 hadi Machi 2026, Serikali imeanzisha kliniki mpya 130 za huduma za kisukari na shinikizo la damu, na kufanya idadi ya kliniki hizo kufikia 168 kutoka kliniki 38 zilizokuwepo katika kipindi kama hicho mwaka 2025.

Kwa mujibu wa Waziri huyo, kliniki hizo zimepatiwa dawa muhimu, vifaa tiba pamoja na mafunzo kwa watumishi wa afya ili kuboresha upatikanaji na ubora wa huduma kwa wananchi wenye magonjwa yasiyoambukiza.

Aidha, amesema Serikali imeendelea kuboresha huduma za kinga na uchunguzi wa magonjwa hayo kupitia kampeni mbalimbali za afya ikiwemo upimaji wa magonjwa yasiyoambukiza katika maeneo ya kazi, utoaji wa elimu kwa jamii pamoja na matembezi ya Kitaifa yanayohamasisha wananchi kufanya mazoezi.

Mchenjgerwa ameongeza kuwa Wizara pia imeendelea kutumia vyombo mbalimbali vya habari kutoa elimu ya uhamasishaji kwa wananchi kuhusu namna ya kujikinga na kudhibiti magonjwa yasiyoambukiza, hatua inayolenga kupunguza ongezeko la wagonjwa na madhara yatokanayo na magonjwa hayo nchini.



Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma 

Serikali kupitia Wizara ya Afya imeendelea kuonyesha mafanikio makubwa katika sekta ya afya baada ya kiwango cha utoaji wa chanjo nchini kufikia asilimia 96, hatua inayotajwa kuwa ni mafanikio makubwa katika kuimarisha kinga dhidi ya magonjwa kwa watoto na wananchi kwa ujumla.

Hayo yameelezwa na Waziri wa Afya, Mhe. Mohammed Mchengerwa (MB), wakati akiwasilisha Bajeti ya Wizara ya Afya kwa mwaka wa fedha 2026/27 bungeni, ambapo amesema ongezeko hilo limetokana na juhudi za Serikali za kuimarisha huduma za msingi za afya pamoja na kuongeza upatikanaji wa chanjo katika maeneo mbalimbali nchini.

Amesema kiwango hicho kimeongezeka kutoka asilimia 93 hadi asilimia 96, jambo linaloifanya Tanzania kuvuka lengo la kimataifa la asilimia 90 lililowekwa kwa ajili ya utoaji wa chanjo.

“Kuongezeka kwa kiwango hiki ni matokeo ya uwekezaji mkubwa unaoendelea kufanywa na Serikali katika sekta ya afya, hususan kwenye huduma za kinga na chanjo ambazo zimeendelea kuwafikia wananchi wengi zaidi mijini na vijijini,” amesema Mchengerwa.

Aidha, Waziri huyo amesema Serikali itaendelea kuboresha mifumo ya utoaji wa chanjo kwa kuhakikisha huduma hizo zinapatikana kwa urahisi katika vituo vya afya, zahanati na hospitali nchini kote ili kuongeza ulinzi dhidi ya magonjwa yanayozuilika kwa chanjo.

Ameeleza kuwa hatua hiyo ni sehemu ya mkakati mpana wa Serikali wa kuimarisha afya ya mama na mtoto pamoja na kupunguza vifo vinavyotokana na magonjwa ya kuambukiza ambayo yanaweza kuzuilika kupitia chanjo.

Mbali na hilo, Serikali imeendelea kuhamasisha wananchi kujitokeza kupata chanjo pamoja na kushiriki katika kampeni mbalimbali za afya zinazolenga kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa kinga na huduma za afya za msingi.

Wadau wa afya wameendelea kuipongeza Serikali kwa hatua hiyo wakieleza kuwa kuongezeka kwa kiwango cha chanjo kutasaidia kujenga jamii yenye afya bora na kupunguza mzigo wa magonjwa nchini.

Kwa mujibu wa wataalamu wa afya, utoaji wa chanjo kwa kiwango kikubwa ni moja ya njia muhimu za kudhibiti magonjwa hatari kwa watoto na jamii kwa ujumla, huku mafanikio hayo yakitajwa kuiweka Tanzania katika nafasi nzuri ya kuendelea kuboresha sekta ya afya na huduma za kinga.








Na Karama Kenyunko Michuzi Tv
FAMILIA bora imeelezwa kuwa msingi muhimu wa kujenga taifa lenye maadili, nidhamu na upendo, huku wazazi na walezi wakitakiwa kuzingatia malezi yenye usawa wa kijinsia na mawasiliano mazuri ili kuhakikisha watoto wanakua katika mazingira salama na yenye ustawi.

Hayo yameelezwa na Mkurugenzi Msaidizi wa Kitengo cha Malezi na Familia kutoka Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Makundi Maalum, Carlos Gwamagobe, wakati akitoa mafunzo katika mafunzo maalum kwa waandishi wa habari za watoto kutoka mikoa mbalimbali nchini yaliyofanyika jijini Dar es Salaam.

Gwamagobe alisema serikali inaendelea kuweka mkazo katika kuhakikisha watoto wanapata malezi bora yanayozingatia upendo, ulinzi, maadili na usawa wa kijinsia kwa kuwa watoto wa leo ndiyo msingi wa maendeleo ya taifa la kesho.

Alisema wazazi wanapaswa kuwa karibu na watoto wao kwa kuwasikiliza, kuwapa muda na kuwalea katika mazingira yasiyo na ukatili ili kuwajengea kujiamini na kukuza ustawi wao.

“Familia bora hujenga watoto wenye maadili mema ambao baadaye huwa wananchi wenye mchango mkubwa katika maendeleo ya jamii na taifa kwa ujumla,” alisema Gwamagobe.

Aidha, alisema ushirikiano kati ya serikali, vyombo vya habari na wadau mbalimbali ni muhimu katika kuhamasisha malezi bora yatakayosaidia kujenga familia imara na watoto wenye maadili mema.

Kwa upande wake, Mratibu wa Programu ya Malezi na Familia kutoka wizara hiyo, Victor Rugarabamu, alisema tafiti zinaonyesha kuwa kukosekana kwa malezi yanayozingatia usawa wa kijinsia ni miongoni mwa sababu zinazochangia kudorora kwa ustawi wa watoto nchini.

Alisema kupitia mafunzo hayo, wizara inatarajia kuona vipindi vinavyorushwa kupitia redio za jamii, televisheni na mitandao ya kijamii vikitoa elimu ya maadili mema, kuhamasisha malezi bora na kuwasaidia watoto pamoja na vijana balehe kukua katika mazingira salama yenye upendo na ulinzi.

“Waandishi wa habari mna nafasi kubwa ya kuelimisha jamii kupitia maudhui wanayoandaa. Tunahitaji vipindi vinavyofundisha, kuburudisha na kujenga maadili kwa watoto,” alisema Rugarabamu.

Naye Mkufunzi wa Malezi ngazi ya Taifa, Sabrina Majikata kutoka Shirika lisilo la Kiserikali la ICS, alisema mafunzo hayo yamejikita katika nguzo kuu tatu za malezi ambazo ni kumjali mtoto, kumlinda na kuzungumza naye kwa karibu.

Alisema wazazi wengi wanakosa muda wa kukaa na watoto wao hali inayochangia kupungua kwa mawasiliano ndani ya familia na kusababisha watoto kukosa nafasi ya kueleza changamoto wanazokutana nazo.

“Mwandishi wa habari anapokuwa na uelewa kuhusu ukuaji wa watoto na changamoto zinazowakabili, anakuwa na uwezo mkubwa wa kuandaa maudhui yenye manufaa kwa jamii,” alisema Sabrina.

Kwa upande wake, Mtaalamu wa Mabadiliko ya Tabia za Jamii kutoka UNICEF, Alice Mwiru, alisema shirika hilo litaendelea kushirikiana na serikali katika kuboresha ustawi wa watoto na kuhakikisha haki zao zinapewa kipaumbele kupitia vyombo vya habari.

Alisisitiza umuhimu wa waandishi wa habari kutumia ubunifu, lugha rafiki kwa watoto na kuzingatia maadili ya taaluma ya habari katika kuandaa vipindi vinavyochangia ukuaji na maendeleo ya mtoto.

Washiriki wa mafunzo hayo wamesema elimu waliyoipata itawasaidia kuandaa maudhui yanayowagusa watoto na vijana kwa njia sahihi na yenye kujenga jamii yenye maadili mema.

“Mafunzo haya yamenipa uelewa mpana kuhusu namna ya kuandaa maudhui yanayofundisha na kuburudisha kwa wakati mmoja huku yakizingatia hatua za ukuaji wa mtoto,” alisema Mika Ndaba






Na Hassan Kimweri, WAF - Dodoma

Sekta ya afya nchini imepata mafanikio makubwa katika kipindi cha awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan yaliyoongeza upatikanaji wa huduma za afya kwa wananchi kupitia ujenzi wa miundombinu, ununuzi wa vifaa tiba, uoatikanaji wa dawa pamoja na huduma za kibingwa na za dharura nchini.

Waziri wa Afya Mhe. Mohamed Mchengerwa amesema hayo leo Mei 11, 2026 wakati akiwasilisha Bajeti ya Wizara ya Afya kwa mwaka wa fedha 2026/27 katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya Spika wa Bunge Mhe. Mussa Azan Zungu.

"Eneo la vituo vya kutolea huduma za afya vimeongezeka kutoka elfu 10,153 mwaka 2021/22 hadi elfu 13,683 kufikia Machi 2026, sawa na ongezeko la vituo 3,530, Zahanati zimeongezeka kutoka elfu 7,189 hadi elfu 8,706 huku hospitali zikiongezeka kutoka mia 404 hadi mia 475 mwaka 2026," amesema Waziri Mchengerwa

Aidha, Waziri Mchengerwa amesema Serikali imeongeza majengo mapya katika hospitali mbalimbali zikiwemo Hospitali ya Muhimbili, KCMC, BMH, Bugando, Mirembe, pamoja na Kibong'oto huku ikiwa imejenga hospitali mpya 10 za rufaa za mikoa, kukarabati hospitali kongwe 50, kukamilisha maboma 980 ya zahanati na kujenga vituo vya afya 390.

Amesema, katika huduma za afya ya uzazi, mama na mtoto, Serikali imeongeza wodi za watoto wachanga kutoka 80 hadi 438 pamoja na vituo vya upasuaji wa dharura kutoka 445 hadi 630 ambayo ni mafanikio yaliyochangia kupungua kwa vifo vitokanavyo na uzazi kutoka vifo 556 mwaka 2016 hadi vifo 104 mwaka 2022 kwa kila vizazi hai 100,000.

"Katika huduma za uchunguzi na matibabu ya kibingwa, Serikali imenunua na kusimika vifaa tiba vyenye thamani ya Shilingi bilioni 241.6 ambapo mashine za MRI zimeongezeka kutoka 7 hadi 13, CT Scan kutoka 12 hadi 45 pamoja na Digital X-ray kutoka 147 hadi 559," amesema Waziri Mchengerea

Kwa upande wa chanjo, amesema watoto waliopata chanjo ya Pentavalent dozi ya tatu wameongezeka kutoka watoto milioni 2,093,412 hadi milioni 3,186,979 huku kiwango cha chanjo kikiongezeka kutoka asilimia 93 hadi 96, juu ya lengo la kimataifa la asilimia 90.

"Upatikanaji wa dawa na bidhaa za afya umeimarika, Serikali imetoa Shilingi trilioni 1.4 kwa ajili ya ununuzi wa dawa na vifaa tiba, viwanda vipya 11 vya dawa na vifaa tiba vimeanzishwa huku 'Tanzania Pharmaceutical Industries kikifufuliwa kwa ajili ya uzalishaji wa dawa za VVU nchini," amesema Waziri Mchengerea


-Wanufaika 463,228 waanza kupata huduma za matibabu.


Na Grace Michael, NHIF-Dodoma

Serikali imeanza rasmi utekelezaji wa Mpango wa Bima ya Afya kwa Wote kwa kaya zisizo na uwezo kwa kutoa Shilingi bilioni 48.8 kwa ajili ya kuwawezesha wananchi wa makundi maalum kupata huduma za afya kwa uhakika.

Kupitia utekelezaji huo, jumla ya kaya 172,297 tayari zimefikiwa na kuingizwa kwenye mpango huo, huku wanufaika 463,228 wakianza kupata huduma mbalimbali za matibabu katika vituo vilivyosajiliwa nchini.

Akiwasilisha Hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Afya Fungu 52 kwa mwaka 2026/27 Waziri wa Afya Mhe. Omary Mchengerwa amesema kuwa, utekelezaji huu unaonesha dhamira ya Serikali ya kuhakikisha kila Mtanzania anapata huduma bora za afya bila kujali hali yake ya kiuchumi, ikiwa ni sehemu ya safari ya kuelekea huduma jumuishi za afya kwa wananchi wote.

Katika kuimarisha sekta ya afya sambamba na utekelezaji wa mpango huo, mabaraza na bodi za kitaaluma yameendelea kusimamia ubora wa huduma kwa kusajili wataalam wa afya 14,310, hatua inayoongeza nguvu kazi muhimu kwa utoaji wa huduma nchini.

Amesema kuwa kuhusu upatikanaji wa huduma za matibabu, jumla ya maduka ya dawa 330 yamesajiliwa pamoja na watarajali 3,004, huku vituo vya kutolea huduma za afya 3,643 vikisajiliwa ili kuongeza upatikanaji wa huduma karibu na wananchi.

Katika kuhakikisha taaluma na maadili yanaendelea kuzingatiwa hususan wakati huu wa kuhudumia wananchi wengi zaidi kupitia mfumo wa Bima ya Afya, vituo binafsi vya afya 654 vimekaguliwa ili kuhakikisha vinakidhi viwango na kutoa huduma salama kwa wananchi.

Mafanikio hayo yanaakisi hatua kubwa ya Serikali katika kujenga mfumo imara wa afya unaojali usawa, ubora na upatikanaji wa huduma kwa wote, huku Bima ya Afya kwa Wote ikiendelea kuwa nguzo muhimu ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi.


Na Janeth Raphael- MichuziTv -Dodoma.

Mbunge wa Kigoma Mjini, Clayton Chipando maarufu kama Baba Levo, ameibua wasiwasi kuhusu kuendelea kwa migogoro ya ardhi nchini, akisema suala hilo limekuwa chanzo kikubwa cha migongano katika jamii kutokana na umuhimu mkubwa wa ardhi katika maisha ya watu.

Akizungumza bungeni, mbunge huyo amesema duniani kuna mambo matatu ambayo watu hupambana nayo kwa nguvu zote ambayo ni fedha, mapenzi na ardhi, akisisitiza kuwa migogoro mingi inayojitokeza nchini inahusishwa moja kwa moja na matumizi ya ardhi pamoja na mabadiliko ya matumizi ya maeneo yaliyotengwa kwa matumizi ya umma.

Mbunge huyo alihoji ni lini Serikali itaweka sheria kali zaidi zitakazodhibiti tabia ya kubadilisha matumizi ya maeneo ya wazi pamoja na maeneo yaliyotengwa kwa huduma za jamii, hali ambayo imekuwa ikichochea migogoro ya mara kwa mara katika maeneo mbalimbali nchini.

“Ardhi imekuwa chanzo kikubwa cha migogoro. Tunaona maeneo ya wazi na yale yaliyotengwa kwa matumizi ya umma yakibadilishwa matumizi kila mara. Serikali ina mpango gani wa kuweka sheria kali kudhibiti hali hii?” alihoji Baba Levo.

Akijibu swali hilo, Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Kaspar Mmuya, alisema Serikali inaendelea kuchukua hatua dhidi ya wote wanaovamia maeneo ya wazi au kuendeleza shughuli za ujenzi bila kufuata sheria, taratibu na mipango ya matumizi ya ardhi iliyowekwa.

Mmuya ametoa onyo kali kwa wananchi wanaojihusisha na ujenzi katika maeneo yaliyotengwa kwa matumizi ya umma bila kibali halali, akisema Serikali haitasita kubomoa majengo yote yaliyojengwa kinyume cha sheria bila kujali gharama zilizotumika katika ujenzi huo.

Alisisitiza kuwa ulinzi wa maeneo ya wazi ni muhimu kwa maendeleo ya miji na ustawi wa jamii, hivyo wananchi wanapaswa kufuata sheria za mipango miji na matumizi bora ya ardhi ili kuepusha migogoro isiyo ya lazima.

Aidha, Serikali imewahimiza wananchi kuhakikisha wanapata vibali na kufuata utaratibu sahihi kabla ya kuanza maendeleo yoyote ya ujenzi ili kulinda maeneo yaliyotengwa kwa manufaa ya umma pamoja na kudumisha utaratibu wa mipango miji nchini.




-Mradi wa Nishati Safi ya Kupikia waongeza ajira kwa vijana

Bodi ya Nishati Vijijini (REB) leo Mei 10, 2026 imefanya ziara katika Kampuni zinazozalisha, kusambaza bidhaa za nishati safi ya kupikia katika Mkoa wa Arusha.

Bodi hiyo ikiwa imeongozwa na Mwenyekiti wake, Mhe. Balozi Meja Jenerali (mstaafu), Jacob Kingu pamoja na Wajumbe wa Bodi hiyo, Mhe. Radhia Msuya na Mhandisi Sophia Mgonja waliweza kutembelea kampuni ya Ignate Energy Access yenye bidhaa za My Sol pamoja na kampuni ya HannyG Investment.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mwenyekiti Kingu, amezipongeza kampuni hizo kwa kuunga mkono kampeni ya Serikali ya Nishati Safi ya Kupikia kwa kuanza kutengeneza pamoja na kusambaza bidhaa za nishati safi ya kupikia huku akitoa wito kwa makampuni mengine kuendelea kuunga mkono kampeni hiyo ili malengo yaliyowekwa ya ifikapo 2034, Asilimia 80 ya Watanzania wawe wanatumia nishati safi ya kupikia.

Awali akitoa taarifa ya utendaji wa kampuni ya My Sol, Meneja Uendeshaji wa Mitambo, Joe Chambua, amesema kuwa pamoja na huduma zingine zinatolewa na kampuni hiyo ikiwamo huduma ya ufungaji wa umeme jua, kampuni hiyo imeanza kutekeleza mradi wa nishati safi ya kupikia kwa kuja na teknolojia rahisi na ya gharama nafuu ya mtambo wa biogasi.

Amesema kuwa wamefanikiwa kufunga mitambo ya biogasi katika taasisi mbalimbali nchini ikiwemo Magereza.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Msaidizi wa kampuni ya Hanny G Investment, Hanny Mbaria, ambao wanajishughulisha na utengenezaji wa majiko banifu pamoja na mkaa mbadala ameishukuru Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kwa kuipa kampuni hiyo kazi ya kusambaza majiko banifu na mkaa mbadala katika shule 53 Tanzania Bara.

Mbaria amesema licha ya mradi wa nishati safi ya kupikia kulinda mazingira lakini pia mradi huo umetoa ajira kwa vijana wengi.

“Kwa sasa kampuni yetu imekua zaidi na tumeajiri vijana wengi zaidi tofauti na hapo awali. Kwa sasa tuna wafanyakazi zaidi ya 120 wenye ajira za kudumu na wasio na ajira za moja kwa moja ni 1000,” amesema Mbaria.


Kampuni ya mawasiliano ya Yas imefungua rasmi duka jipya la huduma katika eneo la Nungwi, Mkoa wa Kaskazini Unguja, hatua inayolenga kurahisisha upatikanaji wa huduma za mawasiliano na kifedha kwa wakazi wa Zanzibar.

Uzinduzi huo umefanyika hivi karibuni eneo la Nungwi - Zanzibar na kuongozwa na Mstahiki Meya wa Baraza la Manispaa ya Wilaya ya Kaskazini A’ Unguja, Mhe. Nyange Kher Ali, aliyemwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Unguja.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mhe. Nyange Kher Ali aliipongeza Yas kwa kuendelea kuwekeza Zanzibar na kusaidia jitihada za Serikali katika kuboresha huduma za mawasiliano pamoja na kuongeza fursa za ajira kwa vijana.

“Uwekezaji huu una mchango mkubwa katika kukuza uchumi wa wananchi wetu pamoja na kuongeza upatikanaji wa huduma muhimu za kidijitali,” alisema Mhe. Nyange Kher Ali.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Huduma kwa Wateja na Uendeshaji wa Yas, Bi. Mwangaza Matotola, alisema kufunguliwa kwa duka hilo ni sehemu ya mkakati wa kampuni wa kusogeza huduma karibu zaidi na wananchi na kuendelea kuimarisha uchumi wa kidijitali nchini.

“Uzinduzi wa duka hili hapa Nungwi ni sehemu ya mkakati wetu wa kuhakikisha kila Mtanzania anapata huduma za mawasiliano na kifedha kwa urahisi, haraka na kwa viwango vya hali ya juu,” alisema Bi. Matotola.

Alisema Yas imeendelea kuwekeza katika upanuzi wa miundombinu yake nchini kupitia teknolojia za 4G na 5G, huku kampuni hiyo ikiwa na zaidi ya minara 4,800 inayohudumia zaidi ya wateja milioni 31 Tanzania Bara na Zanzibar.

Bi. Matotola alisema Nungwi ni eneo muhimu kiuchumi kutokana na shughuli za utalii, uvuvi na biashara, hivyo uwepo wa duka hilo utasaidia wananchi na wafanyabiashara kupata huduma kwa ukaribu zaidi.

Aidha, aliwahamasisha wananchi kutumia applikesheni mpya ya Yas inayowezesha upatikanaji rahisi wa huduma mbalimbali kidijitali.

Duka la Nungwi linaungana na mtandao wa zaidi ya maduka 556 ya Yas yaliyopo nchini kote, yakilenga kuboresha huduma kwa wateja na kuongeza upatikanaji wa huduma za kidijitali kwa Watanzania.






Standard Chartered Tanzania iliandaa tukio maalum la kutazama mubashara mechi iliyokuwa ikisubiriwa kwa hamu kubwa ya Ligi Kuu England kati ya Liverpool FC na Chelsea FC siku ya Jumamosi, tarehe 9 Mei 2026.

Tukio hilo lililofanyika Bravo Coco jijini Dar es Salaam, liliwakutanisha wanachama wa Klabu ya Mashabiki wa Liverpool FC nchini pamoja na baadhi ya wateja wa Standard Chartered kwa alasiri ya kipekee iliyojawa na burudani ya soka, urafiki na mshikamano wa kijamii. Tukio hili lilikuwa sehemu ya dhamira endelevu ya Benki ya kuimarisha mahusiano na wateja wake pamoja na kusherehekea ushirikiano wake wa kimataifa na Liverpool FC kwa njia yenye maana kwa jamii ya hapa nchini.

Eneo la tukio lilipambwa kwa mandhari ya kuvutia yaliyochochewa na uwanja wa Anfield, yakiambatana na mapambo maalum, maswali ya maarifa kuhusu klabu, pamoja na zawadi zenye nembo — yote yakilenga kuboresha uzoefu wa watazamaji na kuenzi mapenzi ya mashabiki wa Liverpool nchini Tanzania.

“Soka lina namna ya kipekee ya kuwaunganisha watu, na tunafurahia kuunda nyakati zinazotuunganisha na wateja pamoja na jamii zetu nje ya shughuli za kibenki. Tunathamini fursa zinazotuwezesha kuhusiana zaidi ya huduma za benki, kuimarisha mahusiano na kuunda kumbukumbu nzuri na jamii tunazozihudumia,” alisema George Binde, Afisa Mkuu wa Fedha wa Standard Chartered Bank Tanzania.

Standard Chartered inaendelea kutumia ushirikiano wake wa kimataifa katika michezo kujenga mahusiano ya kudumu na kutoa thamani ya kipekee kwa wateja na jamii katika masoko yake mbalimbali.







• Service revenue surged by 21.8%, underpinned by growth in customers and increased service uptake.

• Underlying net profit crossed the TZS 200 billion mark, a 125.5% growth YoY.

• Record high capex investment of TZS 323.9 billion, an increase of 85.1% YoY, dedicated to broadband coverage expansion and technology infrastructure modernization.

• Solid momentum in driving financial inclusion:

o More than TZS 3 trillion micro loans were disbursed

o M-Koba deposits grew more than 80%, surpassing a trillion shillings

o M-Wekeza provided an investment option for thousands of customers, with total investment exceeding TZS 370 billion in less than 2 years.

Vodacom Tanzania PLC today announced strong profit growth for the financial year ended March 2026, demonstrating excellence in strategy execution, disciplined cost management and sustained investment in network and mobile money platform. The performance was driven by solid service revenue growth and expanding products adoption across all segments.

The results underline Vodacom’s continued focus on profitable growth and long‑term value creation, while maintaining consistent investment to strengthen network quality, expand digital services and support inclusive economic development in Tanzania.

As the only publicly listed telecommunications company in the country, Vodacom highlighted its consistent financial performance and transparency despite ongoing geopolitical pressures and industry disruptions. The company reaffirmed its role as a credible, reliable corporate partner and a responsible contributor to national development, having operated continuously in Tanzania under the Vodacom brand for 25 years.

Speaking on the preliminary financial results for the year ended March 2026, Vodacom Tanzania’s Chief Executive Officer, Philip Besiimire, said the company delivered sustained profitability supported by excellent strategy execution and stable business environment.

Service revenue grew by 21.8% to TZS 1.85 trillion, underpinned by growth in customers and increased service uptake. As a result, net profit after tax increased by 18.4% to TZS 107.1 billion, with an underlying net profit of TZS 204.1 billion excluding temporary one-off cost relating to radio access network modernization. This reflects continued momentum across Vodacom’s core revenue streams and robust cost containment.

“Our strong performance reflects deliberate investment choices and our continued focus on scaling services that deliver value for both our customers and shareholders. Our customer base grew 22.3% and we sustained our position as the market leader,” said Besiimire.

The CEO further detailed “M‑Pesa revenue grew by 24.5%, driven by increased adoption of our services like lending, savings and merchant payments, while data revenue grew by 29.5% a result of increased data customers and smartphone users, supported by investments”.

Guided by its purpose of connecting Tanzanians for a better future, Vodacom continued to invest in social impact initiatives, including free health check camps, ICT modernization in schools, tree‑planting programmes and the Twende Butiama cycling tour, strengthening community engagement and social impact.

Looking ahead, Vodacom Tanzania will continue to prioritize investment in network infrastructure, expansion of financial and enterprise services and enhancement of customer experience. Moreover, the company aims to further align its strategy with Tanzania’s national development plans and digital transformation agenda, leveraging its technology leadership and strong market position.

The CEO reaffirmed Vodacom’s commitment to sustainable growth, ethical operations, environmental stewardship and maintaining trust while expressing confidence that ongoing infrastructure investments will deliver long‑term value for customers, shareholders and the nation.

“As we look to the future, we remain committed to partnering with government and stakeholders to support Tanzania’s development agenda and build a digitally inclusive society,” concluded Mr Besiimire.

Full results: www.vodacom.co.tz/financials






Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb) amewasilisha Ujumbe Maalum kutoka kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa Rais wa Jamhuri ya Djibouti Mhe. Ismaïl Omar Guelleh wa nchi hiyo.

Mheshimiwa Kombo amewasilisha ujumbe huo wakati wa sherehe za uapisho wa Mheshimiwa Rais Guelleh zilizofanyika Mei 09, 2026 jijini Djibouti.




 Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, amemtembelea na kumjulia hali, Katibu Mkuu Mstaafu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na aliyewahi kuwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mzee Yusuph Makamba katika makazi yake Tegeta Jijini Dar es Salaam leo tarehe 10 Mei 2026.




 

MAMIA ya wananchi wamejitokeza  kuchangia damu  katika  kambi maalumu  iliyoandaliwa na Mbunge wa  Jimbo la Ukonga,  Bakari Shingo, viwanja vya Pugu Kajiungeni, wilayani Ilala, jijini Dar es Salaam, leo.

Kambi hiyo  ilianza kwa matembezi ya hisani  ya kilometa tano yaliyoanzia Mombasa  hadi viwanja vya Pugu yakiongozwa na mbunge huyo  na kushiriki, wananchi, vikundi vya jogging na makundi mbalimbali.

Akizungumza katika kambi hiyo, Mbunge Shingo, amesema dhamira ni kuchangisha damu ili kuokoa maisha ya  watu hususan wanawake wanao jifungua, waliopata ajali, wagonjwa wa kawaida na wananchi wote  wenye matatizo ya kuhitaji damu hospitalini.

 Shingo amesema  kuchangia damu ni ibada  hivyo kuwataka wananchi kuendeleza utamaduni huo bila kujali itikadi zao za kidini na kisiasa.

“Damu hii tunayo change itakwenda kuokoa wananchi wote bila kujali dini zao wala itikadi za kisiasa.  Ofisi ya Mbunge Jimbo la Ukonga tunawashukuru wananchi waliojitokeza  leo kujitoleaa damu,”amesema Shingo.

 Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo, ambaye ni Katibu Tarafa ya Ilala, Kheri William, amempongeza Mbunge Shingo kwa kuandaa kambi hiyo na kuomba utaratibu  huo uendelezwe.

“Tunaomba mbunge  huu utaratibu ulioanzisha wa kuandaa matembezi na uchangiaji damu  uendelee. Angalau kila baada ya miezi sita tuandae kambi hii,”alisema Katibu  tarafa huyo.
Alisema katika matibabu damu haina mbadala kwani haitengenezwi  kwa namna yoyote  ispo kuwa kwa wananchi kujitolea damu yao na kuokoa maisha ya wahitaji.

Zoezi la utoaji damu lilisimamia na  maofisa  wa Mpango wa Taifa wa Damu Salamaa, kutoka Hospitali ya Rufani ya Amana, ambao wamempongeza Mbunge Shingo na wananchi wote walio fika kujitolea damu kwa kuzingatia umuhimu wa uchangiaji huo









 

▪️Kumuwakilisha Rais Dkt. Samia mkutano wa ushirikiano wa Afrika na Ufaransa.

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, leo Mei 10, 2026 amewasili Nairobi, Kenya ambako anatarajia kumuwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika Mkutano wa Ushirikiano wa Afrika na Ufaransa (Africa Forward: Africa–France Partnership for Innovation and Growth Summit) utakaofanyika Mei 11–12, 2026.

Lengo la mkutano huo ni kuendelea kuimarisha ushirikiano kati ya Afrika na Ufaransa katika sekta mbalimbali ikiwemo biashara, teknolojia, nishati, afya, Akili Unde (AI), kilimo, uchumi wa buluu pamoja na viwanda.

Aidha, mkutano huo unalenga kukuza uwekezaji mpya kati ya Afrika na kampuni za Ufaransa, kujenga ushirikiano unaotajwa kuwa wa usawa, pamoja na kujadili mageuzi ya mfumo wa fedha na maendeleo endelevu ya Afrika.

Mkutano huo wa Wakuu wa Nchi na Serikali unawakutanisha wadau wa maendeleo, wawekezaji pamoja na sekta binafsi, na umeandaliwa kwa ushirikiano kati ya Rais wa Jamhuri ya Kenya, Mheshimiwa William Samoei Ruto, na Rais wa Jamhuri ya Ufaransa, Mheshimiwa Emmanuel Macron.









Top News