Dkt. Edith Rwiza Mkurugenzi wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia akiongea na Wajumbe wa Baraza la Tatu la Wafanyakazi wa Mamlaka ya Elimu Tanzania wakati alipokuwa anazindua baraza hilo mjini Morogoro.

******************

Na Mwandishi wetu

MOROGORO: Watumishi wa Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) wameagizwa kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao kwa kushiriki kikamilifu katika mijadala ya kikazi, kutoa ushauri wenye tija na kuchangia mawazo yatakayochochea maboresho ya utendaji wa taasisi hiyo pamoja na Serikali kwa ujumla. Wito huo unalenga kuimarisha ushirikishwaji, uwajibikaji na kuongeza matokeo chanya katika sekta ya elimu nchini.

Agizo hilo limetolewa na Mkurugenzi wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Edith Rwiza wakati wa uzinduzi wa Baraza la Tatu la Wafanyakazi wa TEA uliofanyika mkoani Morogoro, ambapo alikuwa Mgeni Rasmi akimuwakilisha Katibu Mkuu wa Wizara hiyo.

Akizungumza katika hafla hiyo, Dkt. Rwiza alisisitiza kuwa TEA ina jukumu muhimu katika kuboresha miundombinu ya elimu nchini ili kuhakikisha upatikanaji wa elimu bora kwa wote. Alieleza kuwa juhudi hizo zinaenda sambamba na utekelezaji wa mtaala mpya unaolenga kukuza umahiri, ubunifu na matumizi ya teknolojia, hivyo kuwahimiza watumishi kuwa wabunifu na wenye kujituma katika maeneo yao ya kazi.

Aidha, alibainisha kuwa kuundwa kwa Baraza la Wafanyakazi ni kielelezo cha ushirikiano mzuri kati ya Menejimenti ya TEA na chama cha wafanyakazi pamoja na uzingatiaji wa sheria za kazi. Alisisitiza kuwa, mabaraza ya wafanyakazi ni vyombo muhimu vya kisheria vinavyotoa fursa kwa watumishi kushiriki katika maamuzi ya kimkakati ya taasisi.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa TEA Dkt. Erasmus Kipesha akiwasilisha taarifa ya mamlaka mbele ya mgeni rasmi alisema kuwa, miongoni mwa majukumu ya Baraza hilo ni kushiriki katika maandalizi ya bajeti, kupokea na kuchambua taarifa za utekelezaji, pamoja na kutoa mapendekezo ya maboresho. Aliongeza kuwa hatua hiyo inasaidia kuwajengea watumishi uelewa mpana kuhusu mwelekeo wa taasisi.

Dkt. Kipesha alieleza kuwa, TEA imeendelea kupata mafanikio makubwa ikiwemo kuimarisha ushirikiano na wadau wa maendeleo. Katika miaka ya fedha 2023/2024 na 2024/2025, mamlaka imetekeleza miradi yenye thamani ya shilingi bilioni 2.15 kwa kushirikiana na wadau wake UNICEF Tanzania, huku katika mwaka wa fedha 2025/2026 miradi yenye thamani ya shilingi bilioni 8.37 ikiendelea kutekelezwa, hususan katika maeneo ya STEM (Sayansi, Teknolojia, Uhandisi, na Hisabati).

Naye mjumbe kutoka Chama cha Wafanyakazi wa Elimu ya Juu Taifa Dkt. Nickson Mkiramweni alisisitiza kuwa, jukumu la kuijenga taasisi ni la wafanyakazi wote hivyo kila mmoja anapaswa kufanya kazi kwa bidii, uaminifu na uzalendo. Alipongeza utendaji wa Baraza la Wafanyakazi la TEA akibainisha kuwa, linaendeshwa kwa misingi ya demokrasia na uwazi hasa katika masuala yanayohusu shughuli za mamlaka hiyo.
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Elimu Tanzania ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi Dkt. Erasmus Kipesha (Kushoto) akisisitiza jambo wakati wa uzinduzi wa Baraza la Tatu la wafanyakazi wa Mamlaka hiyo, mjini Morogoro.Kulia ni Mgeni Rasmi Dkt. Edith Rwiza.
Sehemu ya Wajumbe wa Baraza la Tatu la Wafanyakazi wa Mamlaka ya Elimu Tanzania wakifuatilia hotuba kutoka kwa mgeni rasmi Dkt. Edith Rwiza (hayuko pichani) alipokuwa anazindua baraza hilo mkoani Morogoro.

Mjumbe kutoka Chama cha Wafanyakazi wa Elimu ya Juu Taifa Dkt. Nickson Mkiramweni akitoa salamu kutoka makao makuu ya chama hicho wakati wa uzinduzi wa Baraza la Tatu la wafanyakazi wa Mamlaka ya Elimu Tanzania, mjini Morogoro.
Mkurugenzi wa Huduma za Taasisi Mamlaka ya Elimu Tanzania CPA. Mwanahamis Chambega akieleza jambo wakati wa uzinduzi wa Baraza la Tatu la wafanyakazi wa Mamlaka hiyo, mjini Morogoro. Kushoto ni Mkaguzi wa Ndani CPA. Richard Mazinge






Dar es Salaam, Tanzania
 

Zaidi ya wanafunzi 62,000 kote Tanzania sasa wananufaika na majiko salama na safi zaidi kufuatia usakinishaji wa zaidi ya majiko ya kisasa 170 ya nishati safi ya kupikia katika shule na taasisi za umma zaidi ya 45. Hatua hii muhimu iliadhimishwa katika hafla ya makabidhiano iliyofanyika katika Shule ya Msingi Bunge jijini Dar es Salaam, ikionesha mchango wa mpango huu katika kupunguza matumizi ya kuni na mkaa na hivyo kukabiliana na ukataji wa miti.

Mpango huu unafadhiliwa na Umoja wa Ulaya (EU) na kutekelezwa na Serikali ya Tanzania kwa kushirikiana na Shirika la Umoja wa Mataifa la Maendeleo ya Mitaji (UNCDF) kupitia programu ya CookFund.

Akizungumza katika hafla hiyo, Naibu Waziri wa Nishati, Mheshimiwa Salome Makamba alisema:
“Mapinduzi haya kuelekea matumizi ya nishati safi ya kupikia ni kipaumbele cha kimkakati cha taifa kinachochangia kulinda mazingira, kuboresha afya ya umma na kuongeza ufanisi wa kiuchumi. Kwa kuzipatia shule na taasisi za umma teknolojia za kisasa za kupikia, tunalenga kulinda misitu yetu, kupunguza hewa chafuzi, na kuboresha mazingira ya kujifunzia kwa watoto wetu. Serikali itaendelea kushirikiana na wadau wa maendeleo kupanua upatikanaji wa nishati safi ya kupikia kwa kuzingatia Mkakati wa Taifa wa Nishati Safi ya Kupikia (2024–2034).”

Jitihada za nishati safi ya kupikia nchini zinaongozwa na Wizara ya Nishati kwa kushirikiana na wizara na taasisi nyingine za Serikali, ikiwemo Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Wizara ya Maliasili na Utalii, Ofisi ya Makamu wa Rais – Mazingira, pamoja na taasisi nyingine za umma. Hadi sasa, msaada huu kwa taasisi za umma, hususan shule, unalenga taasisi zote zinazohudumia watu zaidi ya 100 kwa wakati mmoja ili kuachana na matumizi ya kuni na mkaa.

Hatua hizi zinaendana na vipaumbele vya kitaifa vya kupunguza ukataji wa miti, kupunguza uzalishaji wa gesi chafuzi, na kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma za umma. Matumizi ya kuni na mkaa huzalisha chembechembe hatarishi zinazoweza kusababisha magonjwa mbalimbali ya mfumo wa upumuaji kama pumu na saratani ya mapafu.

Kupitia programu ya CookFund, inayofadhiliwa na Umoja wa Ulaya, hatua hizi zinalenga kupunguza matumizi ya nishati za kuni na mkaa kwenda kwenye teknolojia bora na zenye ufanisi zaidi kama majiko yanayotumia mkaa mbadala, majiko ya umeme (electric pressure cookers), biyoethano, majiko banifu, pamoja na gesi. Teknolojia hizi zinatarajiwa kupunguza shinikizo kwa rasilimali za misitu, kuboresha ubora wa hewa jikoni, na kuongeza afya na usalama wa wanafunzi na watumishi. Hadi sasa, taasisi 45 zimeboresha mifumo yao ya upishi, nyingi zikiwa ni shule za msingi na sekondari.

Aidha, kupitia CookFund, UNCDF inatoa msaada wa kifedha na kiufundi kwa makampuni na wajasiriamali wanaokidhi vigezo ili kuongeza usambazaji wa nishati safi ya kupikia. Msaada huu unajumuisha uwekezaji wa mtaji na mtaji wa uendeshaji kwa ajili ya kuimarisha uwezo wa biashara zinazojihusisha na uzalishaji, uagizaji, usambazaji na uuzaji wa majiko, mafuta na bidhaa au huduma zinazohusiana na nishati safi ya kupikia.

Kwa upande wake, Mkuu wa Ushirikiano wa Umoja wa Ulaya nchini Tanzania, Marc Stalmans, alisema:
“Umoja wa Ulaya umejikita kikamilifu katika kuendeleza hatua za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi duniani, na Tanzania siyo tofauti. Mpango huu ni sehemu ya juhudi zetu za kusaidia mpito kuelekea nishati safi. Kupitia msaada wa Umoja wa Ulaya, jamii zinazingatia mbinu endelevu zinazolinda mazingira, huku zikichochea ukuaji wa uchumi, kukuza ajira, na kuboresha upatikanaji wa nishati mashuleni, kwenye biashara pamoja na kaya.”

Naye Mshauri Mkuu Maswala Kiufundi wa UNCDF, Bw. Peter Malika, alibainisha kuwa pamoja na msaada uliotolewa kwa taasisi 45 katika wilaya 14 za Dar es Salaam, Pwani, Morogoro, Dodoma na Mwanza, programu hiyo imewekeza dola milioni 10.1 katika biashara ndogo na za kati 102.

“Nishati safi ya kupikia inapunguza utegemezi wa kuni na mkaa huku ikiboresha usalama, afya na ufanisi wa majiko shuleni,” alisema Bw. Malika. “CookFund inaonesha wazi kuwa teknolojia za kisasa za nishati zinaweza kuleta mageuzi makubwa katika taasisi za umma na kuboresha moja kwa moja mazingira ya kujifunzia kwa maelfu ya wanafunzi.”

Kwa ujumla, programu hii imeleta matokeo chanya na yenye mageuzi makubwa, ikichangia uundaji wa ajira 27,005 (za moja kwa moja na zisizo za moja kwa moja), jumla ya biashara 4,933 katika mnyororo wa thamani wa nishati safi ya kupikia, kufikia kaya zaidi ya 482,089, na kupunguza zaidi ya tani 3,911,450 za uzalishaji wa hewa ukaa. Mafanikio haya yanaonesha mchango mkubwa wa programu hii katika maendeleo endelevu, ustawi wa jamii na hatua za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi nchini Tanzania.Mshauri Mkuu wa Kiufundi wa UNCDF, Bw. Peter Malika, akizungumza wakati wa makabidhiano ya vifaa vya teknolojia ya upishi salama kwa Shule ya Msingi Bunge jijini Dar es Salaam jana. Serikali ya Tanzania, kwa ufadhili wa Umoja wa Ulaya (EU) kupitia Ujumbe wake nchini, na usimamizi wa programu ukifanywa na Mfuko wa Maendeleo wa Mitaji wa Umoja wa Mataifa (UNCDF), inatekeleza Programu ya CookFund ili kuharakisha mpito wa matumizi ya nishati safi ya kupikia katika kaya na taasisi za umma, hususan mashuleni. Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba (wa pili kutoka kulia), alikuwa mgeni rasmi.Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba, akitoa hotuba yake wakati wa makabidhiano ya vifaa vya teknolojia ya upishi salama kwa Shule ya Msingi Bunge jijini Dar es Salaam jana. Serikali ya Tanzania, kwa ufadhili wa Umoja wa Ulaya (EU) kupitia Ujumbe wake nchini, na usimamizi wa programu ukifanywa na Mfuko wa Maendeleo wa Mitaji wa Umoja wa Mataifa (UNCDF), inatekeleza Programu ya CookFund ili kuharakisha kipindi cha mpito wa matumizi ya nishati safi ya kupikia katika kaya na taasisi za umma, hususan mashuleni.Mkuu wa Ushirikiano wa Ujumbe wa EU nchini Tanzania, Bw. Marc Stalmans, akihutubia hadhira wakati wa makabidhiano ya vifaa vya teknolojia ya upishi salama kwa Shule ya Msingi Bunge jijini Dar es Salaam jana. Serikali ya Tanzania, kwa ufadhili wa Umoja wa Ulaya (EU) kupitia Ujumbe wake nchini, na usimamizi wa programu ukifanywa na Mfuko wa Maendeleo wa Mitaji wa Umoja wa Mataifa (UNCDF), inatekeleza Programu ya CookFund ili kuharakisha kipindi cha mpito wa matumizi ya nishati safi ya kupikia katika kaya na taasisi za umma, hususan shule. Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba (wa tatu kutoka kulia), alikuwa mgeni rasmi.Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba (kushoto), anapika wali akitumia jiko linalotumia nishati salama ya kupikia, wakati wa hafla ya makabidhiano ya vifaa vya teknolojia ya upishi salama katika Shule ya Msingi Bunge jijini Dar es Salaam jana. Serikali ya Tanzania, kwa ufadhili wa Umoja wa Ulaya (EU) kupitia Ujumbe wake nchini, na kwa usimamizi wa programu kutoka Mfuko wa Umoja wa Mataifa wa Kuendeleza Mitaji (UNCDF), inatekeleza Mpango wa CookFund ili kuharakisha kipindi cha mpito cha matumizi ya upishi safi katika kaya na taasisi za umma, hususan mashuleni. Kutoka kulia ni Bw. Marc Stalmans, Mkuu wa Ushirikiano wa Umoja wa Ulaya (EU) nchini Tanzania, akiwa pamoja na Mshauri Mkuu wa Kiufundi wa UNCDF, Bw. Peter Malika.

Na Mwandishi wetu -  Dodoma

Jeshi la Magereza Tanzania limehimiza matumizi sahihi ya takwimu za wafungwa na mahabusu kama nyenzo muhimu ya kupanga na kuboresha huduma za urekebishaji.

Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Jeshi la Magereza, CGP Jeremiah Yoram Katungu, Kamishna wa Sheria na Uendeshaji wa Magereza, CP Nicodemus Tenga, amesema takwimu hizo si tu ni hitaji la kitaifa bali pia zinazingatia viwango vya kimataifa vinavyolenga kuongeza uwazi na ufanisi katika taasisi za magereza.

Ameeleza kuwa uwepo wa takwimu sahihi husaidia kupanga mikakati madhubuti ya kuwahudumia wafungwa na mahabusu, ikiwemo masuala ya afya, makazi, lishe na programu za urekebishaji. Pia hutoa mwanga kwa watunga sera kutambua changamoto na kuzitatua kwa wakati.

CP Tenga amesisitiza wataalamu wa takwimu kuhakikisha taarifa wanazokusanya zinatumika kwa vitendo, akibainisha kuwa takwimu zisipotumika hupoteza maana na thamani yake kwa taifa.

Kwa upande wake, Mkuu wa Tafiti na Takwimu wa Jeshi la Magereza, DCP Justine Kaziulaya, amesema mwaka 2025 jumla ya wafungwa na mahabusu walifikia 23,940, ambapo wafungwa walikuwa 19,646 na mahabusu 4,294.

Aidha, amebainisha mikakati mbalimbali ya kupunguza uhalifu ikiwemo utoaji wa mafunzo ya ufundi, programu za kisaikolojia, tiba ya uraibu pamoja na kuimarisha ushirikiano na jamii na matumizi ya teknolojia za kisasa.

Naye Meneja wa Tafiti na Ubunifu kutoka Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS), Bi. Mariam Kitembe, amesema serikali inaendelea kuimarisha sekta ya takwimu kupitia mpango wa TSMP II, ambao unalenga kuongeza ubora na matumizi ya takwimu katika taasisi mbalimbali zikiwemo magereza.


 

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi akizungumza leo Machi 27, 2026 jijini Dar es Salaam katika Mkutano wa Uhakiki wa Rasimu ya Mpango wa Pili wa Kuboresha Mazingira ya Biashara na Uwekezaji (MKUMBI II).
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-Mipango na Uwekezaji, Prof. Kitila Mkumbo, akizungumza leo Machi 27, 2026 jijini Dar es Salaam katika Mkutano wa Uhakiki wa Rasimu ya Mpango wa Pili wa Kuboresha Mazingira ya Biashara na Uwekezaji (MKUMBI II).


Na Mwandishi Wetu
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi, amesema Mpango wa Kuboresha Mazingira ya Biashara na Uwekezaji (MKUMBI) umeendelea kuwa nyenzo muhimu katika kuimarisha mazingira ya uwekezaji na biashara nchini, hatua inayochochea ukuaji wa uchumi na kuvutia wawekezaji wa ndani na nje.

Dk. Mwinyi ameyasema hayo Machi 27, 2026 jijini Dar es Salaam wakati akizungumza katika Mkutano wa Uhakiki wa Rasimu ya Mpango wa Pili wa Kuboresha Mazingira ya Biashara na Uwekezaji (MKUMBI II), ambapo alieleza kuwa mpango huo umewezesha sekta mbalimbali kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi katika kuweka mazingira rafiki ya biashara.

Amesema kupitia maboresho hayo, Serikali imeendelea kuweka misingi imara ya kuvutia uwekezaji huku ikilenga kufikia malengo ya Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 inayokusudia kuifikisha Tanzania kwenye uchumi wa kipato cha juu.

Kwa mujibu wa Dk. Mwinyi, dira hiyo inalenga kufikia uchumi wenye thamani ya dola za Marekani trilioni moja pamoja na kipato cha wastani wa dola 7,000 kwa kila Mtanzania ifikapo mwaka 2050.

Amesisitiza kuwa ili kufikia malengo hayo, nchi inalazimika kuhakikisha ukuaji wa Pato la Taifa unafikia angalau asilimia 10 kwa mwaka kuanzia 2026 hadi 2050, jambo litakalowezekana kupitia uwekezaji mkubwa katika sekta za uzalishaji, viwanda, kilimo cha kisasa, uchumi wa buluu, nishati na TEHAMA.

“Ni wazi kuwa Serikali pekee haiwezi kufanikisha malengo haya, hivyo ushiriki wa sekta binafsi ni muhimu sana katika kuongeza uzalishaji, ajira na mapato ya taifa,” alisema.

Aidha, amebainisha kuwa takwimu zinaonesha mafanikio ya maboresho ya mazingira ya biashara, akitolea mfano mwaka 2024 ambapo miradi 901 ya uwekezaji yenye thamani ya dola bilioni 9.3 ilisajiliwa na kuzalisha ajira zaidi ya 212,000.

Ameongeza kuwa katika kipindi cha miaka miwili ya 2024 hadi 2025, miradi 1,828 yenye thamani ya dola bilioni 20.3 ilisajiliwa nchini, hatua inayodhihirisha kuimarika kwa mazingira ya uwekezaji.

Dk. Mwinyi amesema Serikali pia imeendelea kuwekeza katika miundombinu ya kimkakati ikiwemo reli ya kisasa, bandari, barabara, nishati na TEHAMA ili kupunguza gharama za uzalishaji na kuongeza ushindani wa uchumi.


Amesema kupitia MKUMBI, Serikali imefanya mapitio ya sheria zaidi ya 94 na kuondoa au kupunguza zaidi ya tozo na ada 628 zilizokuwa kikwazo kwa wafanyabiashara, hatua iliyosaidia kupunguza urasimu na kuongeza uwazi katika utoaji wa huduma.

Kwa upande wake, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, Prof. Kitila Mkumbo, amesema mafanikio ya kuboresha mazingira ya biashara yatategemea pia mabadiliko ya mitazamo kwa watendaji wa serikali wanaosimamia utekelezaji wa sera na sheria.

Amesema rasimu ya MKUMBI II imebainisha changamoto 59 zinazokwamisha biashara Tanzania Bara na Zanzibar na kupendekeza maeneo 11 ya mageuzi yenye hatua 246 za utekelezaji ili kuboresha zaidi mazingira ya biashara.

Naye Waziri wa Kazi na Uwekezaji Zanzibar, Shariff Ali Shariff, amesema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeanza kufanya mapitio ya Sheria ya Uwekezaji ya mwaka 2003 pamoja na kuanzisha mifumo ya kidijitali ili kurahisisha huduma kwa wawekezaji wa ndani na nje.

Aidha, baadhi ya wafanyabiashara waliohudhuria mkutano huo walisisitiza umuhimu wa kuondoa vikwazo vinavyokwamisha biashara katika ngazi za halmashauri pamoja na kuhakikisha sekta binafsi inashirikishwa kikamilifu katika utekelezaji wa mpango huo.

Mkutano huo ulilenga kukusanya maoni ya wadau mbalimbali kabla ya kupitishwa kwa rasimu ya mwisho ya MKUMBI II, ambayo inatarajiwa kuwa chombo muhimu katika kuimarisha mazingira ya uwekezaji na kukuza uchumi wa Tanzania.



Matukio mbalimbali katika picha.




Picha za Pamaoja.
Naibu Gavana, Dkt. Yamungu Kayandabila, akijadiliana jambo na Profesa Zhiguo He kutoka Chuo Kikuu cha Stanford Marekani, baada ya ziara ya wanafunzi wa chuo hicho katika ofisi za Benki Kuu jijini Dar es Salaam. Kulia ni Mkurugenzi wa Mifumo ya Malipo ya Taifa, Bi. Lucy Shaidi.

*******************

Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) anayeshughulikia Sera za Uchumi na Fedha, Dkt. Yamungu Kayandabila, amesema kuwa mifumo ya malipo ya Taifa ina mchango mkubwa katika kukuza uchumi jumuishi na kuimarisha ujumuishwaji wa kifedha nchini.

Akitoa hotuba ya ukaribisho kwa wanafunzi wa Shahada ya Uzamili ya Biashara (MBA) kutoka Chuo Kikuu cha Stanford, Marekani, waliotembelea BoT jijini Dar es Salaam, Dkt. Kayandabila alieleza kuwa mifumo ya malipo inachangia ukuaji wa uchumi shirikishi kwa kuwezesha malipo ambayo yanachochea ugavi katika uchumi na kuwa uti wa mgongo wa Uthabiti wa Sekta ya Fedha.

Alibainisha kuwa mifumo ya malipo yenye ufanisi, iliyo salama na shirikishi huchochea ufanisi wa sera ya fedha kwa kuwezesha uenezaji mzuri wa mabadiliko ya viwango vya riba vya Benki Kuu na kuimarisha udhibiti wa ukwasi ndani ya uchumi.

Dkt. Kayandabila alisema Benki Kuu imeendelea kuchukua hatua mbalimbali za kisera na kuwekeza katika miundombinu ili kuimarisha na kuboresha mifumo ya malipo, sambamba na kuchochea ubunifu hususan katika huduma za kifedha za kidijitali na ujumuishwaji wa kifedha.

Akifafanua kuhusu historia ya maboresho hayo, alisema kuwa mchakato wa kisasa wa mifumo ya malipo ulianza katikati ya miaka ya 1990 kama sehemu ya mageuzi mapana ya sekta ya fedha yaliyolenga kuongeza ufanisi, usalama na uthabiti wa mfumo wa fedha.

Aliongeza kuwa mageuzi hayo yaliwezesha kuingia kwa benki binafsi za ndani na za kimataifa, ubinafsishaji wa baadhi ya benki za serikali pamoja na kuondolewa kwa baadhi ya vikwazo katika huduma na bidhaa za kifedha.

Kwa mujibu wa Dkt. Kayandabila, mwaka 1996 BoT ilianzisha Mradi wa Maboresho ya Mifumo ya Malipo ya Taifa uliolenga kubadilisha mfumo wa zamani uliotegemea zaidi fedha taslimu na karatasi kuwa mfumo wa kielektroniki unaoendana na viwango vya kimataifa.

Alikumbusha kuwa kabla ya maboresho hayo, matumizi ya fedha taslimu yalitawala, huku hundi zikichukua hadi siku 14 kukamilisha miamala mikoani na siku 7 jijini Dar es Salaam, hali iliyokuwa ikichelewesha shughuli za kiuchumi.

Aidha, alisisitiza kuwa BoT inaendelea kufuatilia maendeleo ya teknolojia za mifumo ya malipo duniani na kushirikiana na wadau wa kikanda na kimataifa ili kunufaika na ubunifu huo, huku ikiendelea kulinda uthabiti wa sekta ya fedha, uadilifu wa mifumo na maslahi ya watumiaji.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Mifumo ya Malipo ya Taifa, Bi. Lucy Shaidi, akielezea hatua muhimu zilizofikiwa katika safari ya kuendeleza mifumo ya malipo hadi kufikia mwaka 2025, alisema kuwa kumekuwapo na ukuaji wa kasi wa malipo ya papo kwa papo, huduma za fedha kupitia simu za mkononi, pamoja na mifumo ya malipo inayoweza kuunganishwa.

Alibainisha kuwa maendeleo hayo yanaendelea kuichochea Tanzania kuelekea katika mfumo wa fedha uliojumuishi zaidi, wenye ufanisi, na unaotegemea kwa kiasi kikubwa teknolojia za kidijitali.

Miongoni na mafanikio makubwa ya Benki Kuu katika mifumo ya malipo ni kuanzishwa kwa Mfumo wa Malipo ya Papo kwa Hapo (Tanzania Instant Payment System – TIPS) unaoruhusu watumiaji wa huduma za fedha kutuma na kupokea fedha papo hapo , bila kujali taasisi ya kifedha wanayotumia.

TIPS umeongeza ufanisi, umepunguza gharama za miamala, na kuimarisha ujumuishwaji wa kifedha kwa kurahisisha miamala ya kifedha kwa watu binafsi na biashara nchini Tanzania.
Naibu Gavana, Dkt. Yamungu Kayandabila, akifafanua jambo kwa wanafunzi wa Shahada ya Uzamili ya Biashara (MBA) kutoka Chuo Kikuu cha Stanford, Marekani, walipotembelea Benki Kuu ya Tanzania jijini Dar es Salaam kujifunza kuhusu Mifumo ya Malipo ya Taifa inayosimamiwa na BoT.
Mkurugenzi wa Mifumo ya Malipo ya Taifa, Bi. Lucy Shaidi, akizungumza wakati wa ziara ya wanafunzi wa Shahada ya Uzamili ya Biashara (MBA) kutoka Chuo Kikuu cha Stanford, Marekani, walipotembelea Benki Kuu ya Tanzania jijini Dar es Salaam kujifunza kuhusu Mifumo ya Malipo ya Taifa inayosimamiwa na BoT.
Mkurugenzi wa Ustawi na Huduma Jumuishi za Fedha, Bw. Kennedy Komba, akizungumza wakati wa ziara ya wanafunzi wa Shahada ya Uzamili ya Biashara (MBA) kutoka Chuo Kikuu cha Stanford, Marekani, walipotembelea Benki Kuu ya Tanzania jijini Dar es Salaam kujifunza kuhusu Mifumo ya Malipo ya Taifa inayosimamiwa na BoT.
Meneja kutoka Kurugenzi ya Mifumo ya Malipo ya Taifa, Dkt. Willian Mng’ong’ose, akizungumza wakati wa ziara ya wanafunzi wa Shahada ya Uzamili ya Biashara (MBA) kutoka Chuo Kikuu cha Stanford, Marekani, walipotembelea Benki Kuu ya Tanzania jijini Dar es Salaam kujifunza kuhusu Mifumo ya Malipo ya Taifa inayosimamiwa na BoT.
Afisa Uhusiano wa Umma kutoka Idara ya Mawasiliano BoT, Bi. Graceana Mahega, akieleza jambo kuhusu makumbusho ya Benki Kuu ya Tanzania kwa wanafunzi wa Shahada ya Uzamili ya Biashara (MBA) kutoka Chuo Kikuu cha Stanford, Marekani, walipotembelea Benki Kuu ya Tanzania jijini Dar es Salaam tarehe 27 Machi 2026.


Na Mwandishi Wetu

WALIMU 150 wa amali kwenye shule za serikali wanaondoka Jumapili kwenda nchini India kwa mafunzo maalum ya amali ambayo yatawawezesha kuongeza ujuzi kwenye taaluma hiyo.

Walimu hao kutoka mikoa mbalimbali nchini waliagwa rasmi jana kwenye hafla maalum iliyohudhuriwa na viongozi mbalimbali wa serikali.

Waliagwa na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolph Mkenda na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, TAMISEMI, Profesa Riziki Shemdoe na Mkurugenzi Mkuu wa Global Education Link, (GEL) Abdulmalik Mollel.

Akizungumzawakati wa hafla ya kuwaaga walimu hao, Profesa Mkenda alisema safari hiyo ni maono ya Rais Samia Suluhu Hassan ambaye amekuwa akisisitiza kuboreshwa kwa elimu ya amali.

Profesa Mkenda alisema kwa kuwa wameanza kutoa mafunzo hayo ya amali ikiwemo kwenda kujifunza kwenye mataifa mbalimbali duniani hakutakuwa na kurudi nyuma.

“Mheshimiwa Rais Samia amesisitiza mara kadhaa kuhusu mafunzo ya amali, anataka kuona tunakwenda mbali zaidi namimi nasema kwa kuwa tumeanza basi hatutarudi nyuma, tutakwenda India na mataifa mbalimbali kujifunza wenzetu wamefanyanini kwenye mafunzo ya amali,” alisema

Aidha, aliwataka walimu hao kujifunza kwa bidii wakiwa nchini India ili watakaporudi wawe mfano kwa walimu wengine ambao hawajapata nafasi hiyo.

“Tunataka kuona mabadiliko makubwa, mtakaporudi watu waone kabisa kwamba kuna watu walikuwa nchini India kwa masomo, mhakikishe shule zinavifaa vya kufundishia masomo ya amali katika ngazi zote,” alisema

“Tunatambua maono makubwa ya rais wetu kwenye masomo ya amali kwa hiyo kazi yetu sisi wasaidizi wake ni kuyatafsiri kwa vitendo kwa kufanya kazi kuhakikisha tunatimiza ndoto hizo kwa kutoa elimu bora na siyo bora elimu,” alisema

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, TAMISEMI, Profesa Riziki Shemdoe alisema kuzingatia nidhamu na maadili watakayofundishwa nchini India kwaajili ya kuja kuleta matokeo chanya kwenye maeneo yao.

“Tunataka mkirudi muwe chachu kwa wengine kutaka nao kwenda India kujifunza, mtushauri tufanye nini ili tuweze kutoa matokeo chanya kwenye maono ya rais Samia,” alisema

Aidha, alisema safari ya walimu hao ni matokeo ya mabadiliko ya mitaala ya elimu yaliyoanza muda mrefu na kuja kutekelezwa na Rais wa awamu ya sita, Rais Samia Suluhu Hassan.

“Mageuzi ya elimu utekelezaji wake ni wa muda mrefu,unamilima na mabonde kwa hiyo ingawa kuna changamoto nyingi lakini sisitutapambana mpaka mwisho hakutakuwa na kurudi nyuma hata siku moja,” alisema Waziri Shemdoe







Dar es Salaam

KAMPUNI ya Airtel Tanzania imezindua rasmi mnara wa mawasiliano wenye teknolojia ya 4G na 5G katika mtaa wa Machimbo, Tabata, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kampuni hiyo kuboresha huduma za mawasiliano na kukuza uchumi wa kidijitali kwa wananchi.

Akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi, Afisa Mtendaji wa Kata ya Machimbo, Bi. Lidya Bwathondi, alisema kuwa uwekezaji huo umeleta mabadiliko makubwa kwa wakazi wa eneo hilo ambao awali walikumbana na changamoto za mawasiliano.

“Kabla ya ujio wa mnara huu, wakazi wa Machimbo walikuwa wanapata shida kupata mawasiliano ya uhakika. Leo hii hali imebadilika, mawasiliano yameimarika na wananchi wanaweza pia kufanya biashara zao mtandaoni kwa urahisi zaidi,” alisema Bwathondi.

Kwa upande wake, Meneja Biashara wa Airtel, Bw. Benson Mbwanga, alieleza kuwa uzinduzi wa mnara huo ni sehemu ya mkakati wa Airtel wa kuendelea kusogeza huduma karibu zaidi na wananchi pamoja na kuunga mkono jitihada za Serikali katika kuimarisha miundombinu ya mawasiliano nchini.

“Uwekezaji huu unaonesha dhamira ya Airtel ya kuhakikisha kila Mtanzania anapata huduma bora za mawasiliano. Tunaendelea kupanua mtandao wetu wa 4G ili kuwezesha wananchi kuwasiliana kwa urahisi, kufanya biashara za kidijitali na kushiriki kikamilifu katika uchumi wa kisasa,” alisema Mbwanga.

Baadhi ya wakazi wa mtaa wa Machimbo, akiwemo Bi. Mariam Simon, Bi. Bertha Livingston, Bi. Khadija Seif na Bi. Sada Nyambe, walieleza kufurahishwa kwao na uwekezaji huo wakisema utarahisisha shughuli zao za kila siku, hususan biashara za kidijitali, na kuishukuru Airtel kwa kuchagua kuwekeza katika eneo lao.

Uzinduzi wa mnara huu ni sehemu ya uwekezaji mpana wa Airtel ambapo jumla ya minara mipya tisa yenye teknolojia ya 4G imejengwa jijini Dar es Salaam, ikiwa ni jitihada za kuendelea kuboresha huduma za mawasiliano na kusaidia maendeleo ya kijamii na kiuchumi nchini.

Airtel Tanzania inaendelea kujikita katika kutoa huduma bora, za uhakika na zenye ubunifu, huku ikiunga mkono juhudi za Serikali za kuhakikisha upatikanaji wa mawasiliano bora kwa Watanzania wote.




Mbunge wa Jimbo la Kilombero, Abubakari Asenga, ametoa pole kwa wananchi wa jimbo hilo waliokumbwa na mafuriko makubwa yaliyosababishwa na mvua zinazoendelea kunyesha katika maeneo mbalimbali ya Halmashauri ya Mji wa Ifakara, mkoani Morogoro.

Akizungumza leo Machi 27, 2026 katika Ofisi ya Waziri Mkuu inayoshughulikia maafa, Mara baada ya kupokea msaada wa magodoro, mablanketi na chakula, Asenga amesema kuwa juhudi zinaendelea kuhakikisha wananchi waliopata madhara wanapata msaada wa haraka ili kupunguza athari walizokumbana nazo.

Mbunge huyo ameeleza shukrani zake kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, pamoja na Waziri Mkuu, Mwigulu Nchemba, kwa kuwezesha upatikanaji wa vifaa vya dharura kwa ajili ya kuwasaidia waathirika.

Amesema kuwa tayari wamepokea msaada unaojumuisha magodoro 75, mablanketi pamoja na tani 10 za mahindi, ambavyo vitasambazwa kwa wananchi waliokumbwa na mafuriko hayo wakati wakisubiri hatua zaidi za msaada kutoka serikalini.

Aidha, Asenga amewapongeza wananchi pamoja na kamati ya maafa ya wilaya kwa kushirikiana na Jeshi la Zimamoto na Uokoaji kwa juhudi kubwa walizozifanya kuokoa maisha ya watu. Amebainisha kuwa hadi sasa hakuna taarifa yoyote ya vifo iliyothibitishwa licha ya uharibifu mkubwa wa makazi ya wananchi.

Ameongeza kuwa baada ya kupokea taarifa za kuwepo kwa wananchi wasio na mahali pa kulala, ofisi yake ilichukua hatua za haraka kutafuta msaada wa magodoro, mablanketi pamoja na chakula ili kuhakikisha mahitaji muhimu yanapatikana kwa wakati.

Kwa upande mwingine, amesema ofisi ya mbunge imefanikiwa pia kupata unga ambao unatarajiwa kusambazwa kesho Jumamosi katika maeneo yaliyoathirika zaidi ikiwemo Ifakara, Lumemo na Michenga, ili kuwafariji na kuwasaidia wananchi waliokumbwa na adha hiyo.

Asenga amesisitiza kuwa wataendelea kuisimamia serikali kuhakikisha inatekeleza mipango ya kudhibiti athari za mafuriko, ikiwemo kufufua mabwawa, kupanua mito pamoja na kujenga miundombinu ya kinga kama matuta ili kupunguza madhara ya mafuriko siku zijazo.

Kwa mujibu wa taarifa zilizotolewa, takribani kaya 100 zenye jumla ya watu wapatao 500 zimeathirika na mafuriko hayo. Ingawa baadhi ya maeneo yameanza kupungua maji na wananchi kurejea makwao, bado wapo ambao hawajaweza kurudi kutokana na kiwango kikubwa cha maji kilichoingia kwenye makazi yao.

Kwa ujumla, juhudi za serikali zinaendelea kusaidia waathirika wa mafuriko katika Jimbo la Kilombero, huku msisitizo ukiwa ni kuhakikisha misaada ya dharura inawafikia wananchi wote walioathirika na kuweka mikakati madhubuti ya kudhibiti majanga kama haya siku zijazo.





Top News