-Yasema kwa mara ya kwanza Serikali ilikamata tani 29.52 za aina mpya ya dawa za kulevya aina ya Kratom

-Pia mali zenye thamani ya zaidi ya Sh.bilioni 3.3 zilizohusishwa na makosa ya dawa za kulevya zilitaifishwa.


Na Mwandishi Wetu,Michuzi TV

WAZIRI wa Nchi,Ofisi ya Waziri Mkuu(Sera,Bunge,Uratibu na Wenye Ulemavu) Profesa Palamagamba Kabudi ameta taarifa ya hali ya dawa za kulevya kwa mwaka 2025 ambapo inaonesha namna Serikali ya Awamu ya Sita, chini ya uongozi wa Dkt. Samia Suluhu Hassan, ilivyowekeza na kuweka nguvu kubwa katika mapambano dhidi ya dawa za kulevya. 

Akiwasilisha taarifa hiyo leo Mei 29,2029 Bungeni Mjini Dodoma ,Profesa Kabudi amesema uwasilishaji wa taarifa hiyo ni utekelezaji wa Kifungu cha 66 cha Sheria ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya Na. 5 ya Mwaka 2015, inayoiagiza Serikali kuandaa na kuwasilisha bungeni taarifa hiyo kila mwaka.

“Lengo ni kuonesha uwajibikaji wa Serikali kwa wananchi kupitia Bunge, pamoja na kutoa tathmini ya utekelezaji wa mikakati ya udhibiti wa dawa hizo kwa mwaka husika.Pia, taarifa hii inatoa nafasi kwa Bunge kutoa ushauri kwa Serikali kuhusu namna bora ya kukabiliana na tatizo la dawa za kulevya nchini.”

Amefafanua kupitia Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya, vyombo vya ulinzi na usalama, wadau wa ndani na nje ya nchi pamoja na jamii kwa ujumla, serikali imepata mafanikio makubwa katika kudhibiti biashara na matumizi ya dawa za kulevya.Katika taarifa hiyo Profesa Kabudi amesema mwaka 2025, bangi iliendelea kuwa dawa ya kulevya iliyokamatwa kwa kiwango kikubwa zaidi ambapo jumla ya tani 1,017.26, zilikamatwa. 

Amefafanua hata hivyo, kiasi kilichokamatwa kilipungua kwa asilimia 55.97 ikilinganishwa na mwaka 2024.Hiyo ni kutokana na uteketezaji wa mashamba makubwa ya bangi uliofanyika mwaka 2024 na kuimarika kwa udhibiti ikiwemo utoaji elimu kwa jamii inayojihusisha na kilimo cha bangi kuhusu madhara ya kilimo cha zao hilo.

Ameongeza pia jumla ya tani 26.36 za mirungi zilikamatwa. Kiasi hicho kiliongezeka kwa asilimia 42.88 ikilinganishwa na mwaka 2024. Ongezeko hilo linaashiria kuimarika kwa operesheni za ufuatiliaji na udhibiti hususan katika maeneo ya mipaka na njia zinazotumika kusafirisha dawa hizo.

Kwa upande wa dawa za kulevya za viwandani, amesema Serikali ilifanikiwa kukamata methamphetamine kilogramu 907.18, heroin kilogramu 672.23, cocaine kilogramu 4.89, MDMA gramu 178 na MDA gramu 7.82.

Aidha, kwa mara ya kwanza, mwaka 2025 Serikali ilikamata tani 29.52 za aina mpya ya dawa za kulevya aina ya Kratom itokanayo na mmea unaoitwa Mitrogyna speciosa. “Dawa hii iliingizwa nchini kama mbolea, baada ya uchunguzi ilibainika kuwa ni dawa za kulevya.”

Amesema kuwa mafanikio hayo yametokana na kazi kubwa iliyofanywa na Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya kwa kushirikiana na vyombo vyetu vya ulinzi na usalama katika kudhibiti mitandao na njia za usafirishaji wa dawa za kulevya kupitia Nchi kavu, anga na majini.

Aidha, Serikali iliendelea kuimarisha ukaguzi katika vituo vya forodha, vyombo vya usafiri, kampuni za usafirishaji vifurushi na kwenye kampuni zinazojihusisha na biashara ya kemikali bashirifu na dawa tiba zenye asili ya kulevya kwa lengo la kudhibiti uchepushwaji. 

“Kupitia ukaguzi huo, jumla ya tani 31.76 na lita 183.500 za kemikali bashirifu pamoja na kilogramu 2.36 na mililita 160 za dawa tiba zenye asili ya kulevya zilikamatwa.”

Kuhusu makosa ya dawa za kulevya, mwaka 2025,amesema  jumla ya mashauri 1,124 yalifunguliwa katika Mahakama mbalimbali nchini. Pamoja na mashauri yaliyokuwa yakiendelea katika Mahakama mbalimbali nchini, mashauri 1,373 yalitolewa hukumu na Jamhuri ilishinda mashauri 1,058.

Aidha mali zenye thamani ya zaidi ya Tsh. bilioni 3.3 zilizohusishwa na makosa ya dawa za kulevya zilitaifishwa.Pia Serikali iliendelea kutoa huduma za tiba na utengamao kwa watu wenye uraibu wa dawa za kulevya. 

“Mwaka 2025, jumla ya watu 85,425 wenye uraibu wa dawa za kulevya walipata tiba kwenye vitengo vya afya ya akili katika hospitali za rufaa za mikoa na Kanda, kliniki za MAT na nyumba za upataji nafuu nchini.

“Elimu kuhusu madhara ya dawa za kulevya iliendelea kutolewa kwa Umma kupitia kampeni mbalimbali za uelimishaji katika jamii, taasisi za elimu na vyombo vya habari ili kuijengea jamii uelewa, maamuzi sahihi na uwezo wa kujilinda dhidi ya matumizi na biashara ya dawa za kulevya.

“Katika kuimarisha ushirikiano wa kitaifa, kikanda na kimataifa, Serikali imeendelea kushirikiana na wadau mbalimbali wa ndani na nje ya nchi katika kubadilishana taarifa za kiintelijensia, kujenga uwezo wa kitaasisi pamoja na kuendesha operesheni za pamoja dhidi ya mitandao ya usafirishaji na biashara ya dawa za kulevya.

“Matokeo chanya katika mapambano dhidi ya dawa za kulevya yanatokana na dhamira thabiti, maono na uongozi mahiri wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwani chini ya uongozi wake amewekeza kwa kiasi kikubwa katika kufanikisha mapambano dhidi ya tatizo la dawa za kulevya Nchini.”

Pia ameipongeza Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya, vyombo vyetu vya Ulinzi na Usalama, wataalamu wa afya, wadau katika mapambano na wananchi kwa ushirikiano wao uliosaidia kuyafikia mafanikio aliyoyaeleza.

“Naomba wananchi waendelea kutoa taarifa pale wanapohisi au kushuhudia viashiria vya biashara au matumizi ya dawa za kulevya kwa vyombo husika ili kuifanya nchi yetu kuwa mahali salama na huru dhidi ya matumizi na biashara dawa za kulevya.”








Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza wakati wa kikao cha kupokea Taarifa ya Sensa ya Wanyamapori iliyofanyika nchi nzima mwaka 2024 – 2025 iliyowasilishwa na Waziri wa Maliasili na Utalii Dkt. Ashatu Kijaji, tarehe 29 Mei, 2026 Ikulu Dar es Salaam.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye kikao cha kupokea Taarifa ya Sensa ya Wanyamapori iliyofanyika nchi nzima mwaka 2024 – 2025 iliyowasilishwa na Waziri ya Maliasili na Utalii Dkt. Ashatu Kijaji kupitia Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori Tanzania (TAWIRI), tarehe 29 Mei, 2026 Ikulu Dar es Salaam.






 


Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma 

Serikali imesema imeendelea kupata mafanikio makubwa katika vita dhidi ya dawa za kulevya nchini kutokana na kuimarika kwa ushirikiano wa ndani na nje ya nchi pamoja na uwekezaji mkubwa unaofanywa katika sekta ya usalama, intelijensia na udhibiti wa biashara haramu ya dawa hizo.

Hayo yameelezwa leo na  Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Palamagamba John Aidan Mwaluko Kabudi, katika Mkutano na waandishi wa habari Bungeni Dodoma wakati akiwasilisha Taarifa ya Hali ya Dawa za Kulevya nchini kwa mwaka 2025.

Prof. Kabudi amesema Serikali imeendelea kushirikiana na wadau mbalimbali wa kitaifa, kikanda na kimataifa katika kubadilishana taarifa za kiintelijensia, kuendesha operesheni maalum za pamoja pamoja na kujenga uwezo wa taasisi zinazoshughulikia mapambano dhidi ya dawa za kulevya.

Amesema hatua hizo zimeendelea kusaidia kuvunja mitandao ya usafirishaji na biashara ya dawa za kulevya ambayo imekuwa ikihatarisha usalama wa jamii, afya za wananchi na nguvu kazi ya taifa.

Kwa mujibu wa Prof. Kabudi, mafanikio hayo yanatokana na dhamira ya dhati ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, ambaye ameendelea kuimarisha mifumo ya mapambano dhidi ya dawa za kulevya nchini kwa kuongeza uwekezaji katika vyombo vya ulinzi, usalama na taasisi za udhibiti.

Amesema Serikali imeendelea kuiwezesha Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya pamoja na taasisi nyingine zinazoshiriki katika operesheni za kudhibiti biashara hiyo haramu ili kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao.

“Matokeo haya yanaonyesha namna ambavyo ushirikiano wa pamoja kati ya Serikali, vyombo vya dola, wataalamu wa afya, wadau wa maendeleo na wananchi unavyoendelea kuzaa matunda katika vita dhidi ya dawa za kulevya,” amesema Prof. Kabudi.

Aidha, amesisitiza kuwa mapambano dhidi ya dawa za kulevya hayawezi kufanikiwa bila ushiriki wa wananchi, huku akitoa wito kwa jamii kuendelea kutoa taarifa kwa mamlaka husika kuhusu vitendo vinavyohusiana na usambazaji, matumizi au biashara ya dawa za kulevya.

Ameeleza kuwa Serikali itaendelea kuimarisha mikakati ya kinga, elimu kwa umma, tiba na operesheni maalum ili kuhakikisha taifa linaendelea kuwa salama dhidi ya athari za dawa za kulevya ambazo zimekuwa zikichangia mmomonyoko wa maadili, ongezeko la vitendo vya uhalifu pamoja na kuathiri maendeleo ya vijana na jamii kwa ujumla.

Prof. Kabudi pia amewapongeza wananchi kwa ushirikiano wanaoendelea kuutoa kwa vyombo vya usalama na taasisi zinazopambana na dawa za kulevya, akieleza kuwa mchango wa jamii ni msingi muhimu wa ushindi katika mapambano hayo.

Kwa upande wa Kamishina Jenerali Mamlaka ya Kudhibiti na kupambana na Dawa za Kulevya Aretas Lyimo amesema tatizo la dawa za kulevya ni suala  mtambuka linalohusisha mitandao ya kihalifu iliyopo nchi mbalimballi Duniani, hivyo mapambano dhidi ya tatizo hilo yanahitaj ushirikiano na nguvu za pampja kuanzia ngazi ya Kitaifa, kikanfa bna Kimataifa.



 

Mafunzo Elekezi kwa Watumishi Wapya wa Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalum ya Kiuchumi Tanzania (TISEZA) yameanza leo, Mei 28, 2026, ikiwa ni hatua muhimu ya kuandaa wataalamu wa mamlaka hiyo kwa kuzingatia misingi ya utumishi wa umma na miongozo ya serikali. Watumishi wapya 29 wanashiriki mafunzo haya .yanayotolewa na Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC).
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa mafunzo hayo, Mkurugenzi wa Utumishi na Utawala wa Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalum ya Kiuchumi Tanzania (TISEZA) Bi. Anjela Tulumamanywa, alisema kuwa mafunzo elekezi ni nyenzo muhimu kwa wafanyakazi wapya kujifunza misingi ya utumishi wa umma kupitia miongozo mbalimbali ya serikali. 


"Tunatarajia kuwa baada ya mafunzo haya, mtakuwa watumishi wa umma wanaofuata maadili ya utumishi wa umma, wakiwasiliana kwa ufanisi na kuheshimu usiri wa taarifa na nyaraka za serikali, huku pia wakielewa haki na wajibu wao," amesema.

Kwa upande wake, Bi. Zena Hussein ambaye ni Meneja wa kituo cha mafunzo kwa njia ya Mtandao  akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania, amesema kuwa mafunzo haya ni muhimu na lazima kwa watumishi wapya katika utumishi wa umma. 
"Mafunzo haya yanalenga kuimarisha uelewa wa misingi ya utumishi wa umma na miongozo ya serikali, ili kuhakikisha wanatekeleza majukumu yao kwa ufanisi na kwa kuzingatia maadili ya kazi," amesisitiza.

Aidha amesema kuwa Mafunzo haya yanatarajiwa kuongeza uelewa wa watumishi wapya kuhusu misingi ya utumishi wa umma na kuwajengea uwezo wa kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi ndani ya TISEZA. Vilevile, mchakato huo unazingatia taratibu na miongozo ya serikali, kwa lengo la kuhakikisha majukumu yanatekelezwa kwa uwajibikaji, uadilifu, na ufanisi.
Mafunzo haya ni utekelezaji waraka wa Utumishi Na. 5 wa mwaka 2011, uno wataka waajiri kuhakikisha kuwa watumishi wapya wanapatiwa mafunzo elekezi ndani ya miezi sita tangu kuajiriwa,







 

Katibu Mtendaji wa NACTVET Dkt.Mwajuma Lingwanda akizungumza na Waandishi wa habari kuhusiana na kufunguliwa kwa udahili wa wanafunzi katika mwaka wa masomo 2026/2027.




Baadhi ya matukio katika picha wakati wa kutangazwa kwa dirisha la udahili mwaka wa masomo 2026/2027.

Na Mwandishi Wetu
BARAZA la Taifa la Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (NACTVET) limefungua dirisha la Udahili wa wanafunzi kwa mwaka wa masomo 2026/2027 kwa ngazi ya Astashahada na Stashahada katika kozi zote zinazosimamiwa na NACTVET.

Akizungumza na waandishi wa habari mjini Dodoma Katibu Mtendaji wa NACTVET Dkt.Mwajuma Lingwanda amesema dirisha Hilo limefunguliwa rasmi Mei 28 2026.

Amesema maombi ya udahili kwa kozi za Afya na Sayansi Shirikishi -Tanzania Bara, yatafanyika kupitia Mfumo wa Udahili wa Pamoja (CAS) unaopatikana katika tovuti ya Baraza (www.nactvet.go.tz).

Dkt.Mwajuma amesema udahili umeanza Mei 28 hadi Julai 10 2026 kwa awamu ya kwanza.

Aidha amesema maombi ya kozi zisizo za Afya na Sayansi Shirikishi, na kozi za Afya na Sayansi Shirikishi zitolewazo katika vyuo vilivyoko Zanzibar yatumwe moja kwa moja kwenye vyuo husika kuanzia Mei 28 Mei hadi Julai 10 mwaka Hui kwa awamu ya kwanza.

Hata hivyo Baraza limetoa orodha ya kozi zote na vyuo vinavyotoa kozi hizo, inapatikana katika Kitabu cha Mwongozo wa Udahili kwa Mwaka wa Masomo 2026/2027 kinachopatikana katika tovuti ya Baraza (www.nactvet.go.tz).

Baraza hilo limesema kila mwombaji kuhusika mwenyewe katika zoezi zima la kuomba kudahiliwa, kuandika taarifa zake kwa usahihi na umakini, na kutunza kumbukumbu atakazopatiwa na Baraza kupitia namba yake ya simu, bila kumpatia mtu mwingine yeyote ili kuepuka usumbufu unaoweza kujitokeza katika zoezi zima la maombi ya kujiunga na kozi katika vyuo mbalimbali.

Mambo ya Kuzingatia kwa Wanaoomba Kupitia Mfumo wa Udahili wa Pamoja (Central Admission System – CAS) ni Mwombaji anaweza kuomba chuo zaidi ya kimoja na Kuchaguliwa katika chuo alichoomba kutategemea ushindani utakaokuwepo katika chuo hicho.

Aidha amesema mwombaji akishachaguliwa, atapokea ujumbe kutoka NACTVET kupitia namba yake ya simu aliyoweka kwenye mfumo wakati wa kufanya maombi ujumbe utamjulisha kuwa amechaguliwa kujiunga na chuo husika na utakuwa na msimbo (code) ambao atatakiwa kuutunza na kuuwasilisha kwa chuo alichochaguliwa siku atakapowasili chuoni kwa ajili ya kuanza masomo.

Dkt. Mwajuma amesema baada ya kuwasilisha msimbo huo chuoni, atasajiliwa na chuo, kisha atapokea ujumbe kutoka NACTVET ukimweleza kuwa amesajiliwa. Baada ya kusajiliwa, mwanafunzi aingie katika tovuti ya NACTVET (www.nactvet.go.tz), kisha ajiridhishe kuwa amesajiliwa kwa kuhakiki taarifa zake kwa kubonyeza “link” inayosomeka “student’s information verification”.


*Aahidi Kusimama Kidete Iwe Mamlaka

Na Mwandishi Wetu
WAZIRI Mkuu, Dkt Mwigulu Nchemba amezindua mfumo mpya wa kidijitali wa kufuatilia uchafuzi wa mazingira wa Baraza la Taifa la Hufadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC).

Amefanya uzinduzi huo leo Mei 28,2019 jijini Dar es Salaam alipokuwa mgeni rasmi kwenye maadhimisho ya miaka 40 tangu kuanzishwa kwa baraza hilo mwaka 1986.

Maadhimisho hayo ambayo yaliambatana na maonesho ya masuala ya mazingira yamewashirikisha wageni mbalimbali wa serikali na wadau wa sekta binafsi wanaojihusisha na uhifadhi wa mazingira.

Dkt Mwigulu alianza kwa kuipongeza NEMC kwa kazi kubwa ambayo wameifanya kwa miaka yake 40 ya kuhifadhi mazingira akisisitiza kuwa bila mazingira safi binadamu na viumbe wengine wako hatarini kutoweka.

Amesema kazi ya kupambana na waharibifu wa mazingira siyo nyepesi na ndiyo sababu yeye binafsi atasimama kidete kuhakikisha NEMC inakuwa mamlaka ili ipate nguvu ya kukabiliana na wahalibifu wa mazingira.

Aidha, amempongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuwa mwanamazingira namba moja hali ambayo ilifanya atunukiwe tuzo kama kinara wa mazingira duniani kwa kupigia chapuo uhifadhi wa mazingira nchini.

“Mwanamazingira namba moja Rais Dkt Samia Suluhu Hassan amenituma niseme hapa kwamba anatambua mchango wenu na ataendelea kushirikiana nasisi wote kwenye ulinzi wa mazingira, mheshimiwa Rais amekuwa mstari wa mbele kutunza mazingira na ameahidi kuendelea kuwa mstari wa mbele,” amesema Dkt Mwigulu

Amesema ingawa kuna watu wanalichukulia kwa wepesi suala la mazingira lakini tumeanza kuona athari za uhalibifu wa mazingira dhahiri kwenye maeneo mbalimbali nchini.

“Hapo zamani tuliona kama hadithi tu lakini sasa madhara ya kutojali mazingira yameanza kuja kwetu. Hili jambo siyo nadharia na si la kulichukulia kimzaha mzaha hata kidogo na shughuli za binadamu zimeongezeka kwa kasi mno hali ambayo inahatarisha mazingira,” alisema

“Watu wanaamua tu kukata miti ambayo wala wakati mwingine hawana haja nayo baada ya hapo. Mnakata miti mnasababisha jangwa tunakosa maji, mvua hakuna na ushindani wa matumizi ya ardhi unaongezeka kutokana na kuongezeka kwa shughuli za kiuchumi na za binadamu kwa hiyo lazima tukubali kubadilika hatuwezi kwenda na mtindo ule ule wa maisha,” amesema Waziri Mkuu na kuongeza

“Tusipokubali kubadilika tutalazimishwa na yatakayotokea baadae na kwa kuwa NEMC inatakiwa kuwa mamlaka mimi nitasimama kidete iwe mamlaka, mchakato wake utapita Baraza la kazi sasa huko mimi ndiye Mweyekiti nawaaahidi nitalisimamia NEMC iwe mamlaka,”

Aidha, Dkt Mwigulu amesema Rais Samia ameongeza bajeti ya kilimo zaidi ya mara 5 kuwezesha kilimo cha umwagiliaji ili kuondoa mazoea ya wakulima kufyeka mapori na kuharibu mazingira wanapoongeza mashamba.

“NEMC inahitaji kuongezewa meno ili kuongeza ufanisi katika usimamizi wa mazingira na miaka 30 ijayo inakadiriwa kuwa watanzania tutafika milioni 100 na zaidi kwa hiyo lazima NEMC iwe na nguvu kukabiliana na ongezeko la shughuli za binadamu zinazohalibu mazingira,” amesema

“Pamoja na mafanikio tuliyoyapata bado kuna kazi kubwa kufanya mambo makubwa kwenye miaka 40 ijayo. NEMC endeleeeni kutoa elimu ya mazingira kuanzia ngazi ya familia watu wajue umuhimu wa kutunza mazingira,” amesema




Na Karama Kenyunko, Michuzi TV
NDANI ya makasha yaliyojaa taka zinazooza katika maabara ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam Ndaki ya Elimu (DUCE), maelfu ya funza weupe hujificha chini ya mabaki ya vyakula wakila kwa kasi.

Baada ya wiki chache, funza hao hugeuka kuwa chanzo cha protini kwa ajili ya chakula cha kuku, samaki na nguruwe huku wakisaidia kupunguza taka zinazochafua mazingira.

Huo ndio ubunifu wa watafiti wa DUCE waliobuni mradi wa kufuga black soldier fly maarufu kama nzi chuma, wadudu wanaotajwa kuwa sehemu ya suluhu ya changamoto ya chakula cha mifugo na taka ozo mijini.

Pia ubunifu huo unatajwa kuja kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayolenga uchumi wa kisasa, matumizi ya teknolojia, uhifadhi wa mazingira na ajira kwa vijana,

Mtafiti na Mhadhiri kutoka Idara ya Kemia chuoni hapo, Dkt. Lucas Luchemba, anasema walifanya utafiti huo mwaka 2022 baada ya kuona gharama za protini kwenye chakula cha mifugo zikiendelea kuongezeka.

“Tuliangalia kwamba wadudu hawa wanaweza kutoa funza wenye kiwango kikubwa cha protini kati ya asilimia 40 hadi 50 ambazo zinafaa kwa kuku, samaki na mifugo mingine,” anasema.

Kwa mujibu wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO), funza wa black soldier fly wana kiwango kikubwa cha protini kinachowafanya kuwa mbadala wa unga wa samaki (fishmeal) na soya kwenye chakula cha mifugo.

Sekta ya mifugo nchini Tanzania imeendelea kukua sambamba na ongezeko la mahitaji ya nyama, mayai na samaki, lakini gharama ya chakula cha mifugo imeendelea kuwa changamoto kwa wafugaji wengi.

Tafiti zinaonesha kuwa chakula huchukua hadi asilimia 60 hadi 70 ya gharama za uzalishaji wa mifugo huku bei ya fishmeal na soya ikiendelea kupanda.

Utafiti uliochapishwa mwaka 2022 katika jarida la Poultry Science ulionesha kuwa funza wa black soldier fly wana kiwango cha protini kinachofikia asilimia 54.9, kiwango kinachokaribiana na fishmeal yenye asilimia 56 huku kikizidi soybean meal yenye wastani wa asilimia 47.4.

Tofauti na soya inayohitaji ardhi kubwa ya kilimo au fishmeal inayotegemea rasilimali za baharini, funza hao huzalishwa kwa kutumia taka ozo kutoka majumbani, migahawani na masokoni.

Dkt. Luchemba anasema hapo ndipo walipoona suluhu ya protini inaweza pia kuwa suluhu ya mazingira.

Kwa mujibu wa ripoti ya Benki ya Dunia ya mwaka 2020, Dar es Salaam huzalisha takribani tani 4,500 za taka kila siku huku sehemu kubwa ikiwa ni taka zinazooza.

Aidha, Mkakati wa Taifa wa Usimamizi wa Taka Ngumu wa mwaka 2018 ulionesha kuwa taka ozo ni miongoni mwa changamoto kubwa za mazingira katika miji mikubwa kutokana na kuchangia harufu, mafuriko na uzalishaji wa methane.

Methane ni moja ya gesi zinazochochea ongezeko la joto duniani.

“Madampo mengi yanajaa kutokana na taka hizi zinazooza na kutoa harufu kali. Tukiona taka kama rasilimali, tunaweza kupata chakula cha mifugo na wakati huo huo kusaidia mazingira,” anasema Dkt. Luchemba.

Anasema tofauti na nzi wa kawaida wa majumbani, nzi chuma hawana madhara kwa binadamu kwa sababu hawana mfumo wa chakula wala midomo ya kula au kusambaza uchafu.

Safari ya kuzalisha funza hao huanza kwa kupata nzi wazazi wanaotaga mayai.

Dkt. Luchemba anasema nzi hao huwekwa kwenye neti maalum zenye majike na madume ambao hupandiana na kutaga mayai. Harufu ya taka zinazooza huwavutia zaidi kuzaliana.

“Taka huachwa kwa siku nne hadi tano kuoza kabla ya kuwekwa mbao maalum ambazo nzi hutagia mayai,” anasema.

Mayai hayo huwekwa kwenye chombo maalum kilicho juu ya wavu huku chini kukiwa na chakula kama pumba.

Ndani ya siku mbili, mayai hutotolewa na kutoa funza wadogo.

Baadaye funza hao huhamishiwa kwenye makasha yenye taka zilizochakatwa.

“Wanajificha chini ya taka na kuanza kula. Ndani ya wiki moja wanakuwa wakubwa na wazito huku wakiwa wamekusanya protini ya kutosha,” anasema.

Kwa mujibu wake, ndani ya wiki mbili taka nyingi huwa zimevunjwavunjwa huku funza wakipatikana kwa wingi.

Katika uvunaji, asilimia 10 ya funza huachwa kwa ajili ya kuzalisha kizazi kingine huku wengine wakichakatwa kwa matumizi ya chakula cha mifugo.

“Sisi tuna maabara ambayo tunawachakata funza hawa. Tunaweza kuwakausha, kuwasaga kuwa unga laini au kuwauza wakiwa hai,” anasema.

Kwa sasa mradi huo huzalisha kilogramu 300 hadi 400 za funza katika mazingira ya chuo huku kilogramu moja ya funza wabichi ikiuzwa Sh 2,500 na waliokaushwa Sh 5,000.

Kutokana na ongezeko la gharama za chakula cha mifugo, watafiti hao wameanza kutengeneza chakula cha kuku na samaki kwa kuchanganya mahindi, pumba na unga wa funza.

“Tunalenga kupunguza utegemezi wa samaki na soya ambazo gharama zake zimekuwa kubwa,” anasema.

Wataalamu wa mazingira wanaeleza kuwa matumizi ya protini mbadala kama nzi chuma yanaweza kusaidia kujenga mifumo himilivu ya uzalishaji wa chakula kwa kupunguza utegemezi wa malighafi zinazoweza kuathiriwa na mabadiliko ya hali ya hewa.
Mbali na uzalishaji wa chakula cha mifugo, mradi huo pia umegeuka kuwa shamba darasa kwa wanafunzi na jamii.

Dkt. Luchemba anasema tayari wamefikia shule tano za Dar es Salaam pamoja na wanafunzi wa shahada na watu binafsi wanaotaka kujifunza ufugaji wa nzi hao.

“Tunataka kuhakikisha mafunzo ya amali yanafanyika kwa vitendo na vijana wanapata ujuzi wa kujiajiri kupitia teknolojia hii,” anasema.

Anasema ndoto yao ni kuzalisha tani 10 za funza kila mwezi ili kuwafikia wafugaji wengi zaidi pamoja na kusaidia kupunguza taka kwenye madampo.

Mradi huo umewezeshwa na COSTECH kupitia fedha za kuendeleza ubunifu pamoja na mafunzo ya biashara na umiliki wa hati miliki.

Pamoja na mafanikio hayo, changamoto kubwa bado ni uelewa mdogo wa jamii kuhusu matumizi ya wadudu kwenye chakula cha mifugo.

Mkazi wa Dar es Salaam, Angela Mauto, ambaye alianza kufuga nzi hao mwaka 2018 kwa lengo la kupata mbolea, anasema mwanzo watu wengi hawakuelewa kile alichokuwa akifanya.

“Mwanzoni nilipata wakati mgumu kuwaaminisha watu kuwa hiki ni chakula kizuri kwa mifugo. Wengi waliona kama uchafu tu,” anasema.

Anaeleza kuwa wakati mwingine alikuwa akifuga nzi hao ndani ya mazingira ya nyumbani jambo lililozua maswali kutoka kwa watu waliomzunguka.

“Kuna wakati nilikuwa naishi nao kabisa ndani ya nyumba. Jamii ilikuwa hainielewi kutokana na mazingira na eneo nililokuwa nafugia,” anasema.

Licha ya changamoto hizo, watafiti hao wanaamini teknolojia hiyo inaweza kuwa sehemu ya suluhu ya taka, gharama za chakula cha mifugo, ajira kwa vijana na ujenzi wa miji yenye uwezo wa kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Naye Katibu Mkuu wa Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Dkt. Richard Muyungi, anasema Tanzania huzalisha kati ya tani milioni 17 hadi 20 za taka kwa mwaka huku serikali ikiweka mkakati wa kuhakikisha asilimia 70 ya taka hizo zinachakatwa na kurejelezwa ifikapo mwaka 2050.

Amesema ubunifu wa vijana katika kuchakata taka unaweza kusaidia kufanya taka kuwa rasilimali yenye thamani kiuchumi.

Kutoka kwenye taka zinazotupwa kila siku na wengi kuziona kama uchafu, watafiti wanaona fursa ya kuzalisha chakula cha mifugo, kupunguza taka na kufungua njia mpya za ajira kwa vijana. Kile kinachoonekana kuwa mabaki yasiyo na thamani kinaendelea kupewa matumizi mapya kupitia teknolojia inayolenga kukabiliana na changamoto za mazingira na uzalishaji wa chakula.


Na. Hance Mbena - Serengeti

Katika muendelezo wa kuitangaza Tanzania duniani kupitia utalii wa michezo, leo Mei 28, 2026, bingwa wa masumbwi duniani, Terence "Bud" Crawford, amekabidhiwa rasmi ubalozi wa utalii baada ya kukutana na Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Ashatu Kijaji. Tukio hilo limefanyika ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Serengeti ikiwa ni siku ya tano ya ziara yake nchini.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Dkt. Kijaji alieleza kuwa Serikali ya Tanzania chini ya Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, imeendelea kuifungua na kuitangaza sekta ya utalii kimataifa kupitia kampeni mbalimbali za kuitangaza nchi, ikiwemo filamu za “Tanzania: The Royal Tour” na “Amazing Tanzania” ambazo zimeendelea kuvutia wageni na watu mashuhuri kutoka mataifa mbalimbali duniani kutembelea Tanzania.

"Michezo ni sehemu muhimu ya ajira na maendeleo ya uchumi, lakini pia imekuwa daraja la kuunganisha Tanzania na watu mashuhuri duniani. Kupitia michezo tunaendelea kuitangaza Tanzania kimataifa na kufungua fursa mpya za utalii, uwekezaji na ajira kwa vijana,” amesema Waziri Kijaji.

Aidha, Waziri Kijaji alisisitiza kuwa Serikali inatarajia kuendelea kupokea watu mashuhuri kutoka mataifa tofauti duniani watakaotembelea vivutio vya utalii nchini, hatua ambayo itaendelea kuongeza thamani ya utalii wa Tanzania katika soko la kimataifa. Fauka ya hayo Waziri Kijaji amemkabidhi cheti cha kutambua mchango wake na kumpa ubalozi wa kuvitangaza vivutio vya utalii vinavyopatikana nchini kwa mwanamasumbwi huyo.

Kwa upande wake, mwanamasumbwi Crawford amepongeza ukarimu wa Watanzania pamoja na uzuri wa vivutio vya asili alivyovitembelea katika Hifadhi za Taifa Tarangire na Serengeti tangu kuwasili kwake nchini Mei 24, 2026, huku akiahidi kwenda kuwa balozi mzuri wa vivutio vya utalii Tanzania.

Naye, Kamishna wa Uhifadhi, CPA Musa Nassoro Kuji alieleza kuwa utalii wa michezo unaviongezea sifa na kuvitangaza vivutio vinavyopatikana nchini, pia amesisitiza kuendelea na zao hili la utalii wa michezo ambalo litachangia kufungua utalii wa Tanzania duniani, hivyo kuchangia kuongeza pato la Taifa.

Akiwa ndani ya Hifadhi ya Serengeti, bingwa huyo wa masumbwi atashiriki katika shughuli mbalimbali za kitalii zitakazosaidia kuitangaza hifadhi hiyo. Shughuli hizo ni pamoja na utalii wa puto (balloon safari), utalii wa kutumia gari (game drive), pamoja na utalii wa gari nyakati za usiku (night game drive) utakao mpa fursa ya kushuhudia maisha ya wanyamapori katika mazingira yao halisi wakati wa usiku.

Hifadhi za Taifa zimeendelea kuwa sumaku ya kuwavutia watu mashuhuri, wakiongozwa na bondia nguli Terence “Bud” Crawford pamoja na nyota wa zamani wa soka wa klabu ya Manchester United na timu ya taifa ya Uingereza, Rio Ferdinand. Ujio wa magwiji hawa ni kielelezo tosha cha mafanikio ya mkakati wa Serikali, kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii, katika kuunganisha utalii na michezo kuitangaza Tanzania.














-Asema vilifanya kazi kubwa kuhakikisha nchi inaendelea kuwa salama hadi sasa 

-Asisitiza CCM imesikitishwa na vifo 518 vilivyotokea wakati wa vurugu, madhara mbalimbali


Na Said Mwishehe,Michuzi TV.

KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dk. Asha-Rose Migiro amesema sababu kubwa ya chama hicho kupongeza vyombo vya ulinzi na usalama baada ya matukio ya Oktoba 29,2025 ni kutokana na juhudi kubwa zilizofanywa na vyombo hivyo katika kudhibiti vurugu na kulinda usalama wa taifa.

Amesema kazi iliyofanywa na vyombo hivyo Oktoba 29 ndio ambayo imewezesha hadi sasa Taifa la Tanzania kuendelea kuwa Taifa moja na imara licha ya kuwepo kwa dosari katika wakati ule lakini kwa sehemu kubwa vimefanya kazi nzuri ,hivyo wanapongeza.

Dk.Migiro ameyasema hayo leo Mei 28,2026 alipokuwa katika kipindi cha Kasri la Kikeke, ambapo ametumia nafasi hiyo kujibu maswali mbalimbali aliyoulizwa na alijibu kwa ufasaha mkubwa.

Balozi Dk.Migiro amesema  pamoja na changamoto na dosari zilizoweza kujitokeza wakati wa utekelezaji wa majukumu yao, vyombo vya dola vilifanya kazi kubwa kuhakikisha nchi inaendelea kuwa salama katika kipindi kigumu kilichoshuhudia vurugu katika maeneo mbalimbali nchini.

"Pamoja na dosari zilizoweza kujitokeza wakati wa utekelezaji wa majukumu yao, bado kazi kubwa iliyofanywa na vyombo vya dola ilisaidia kuzuia madhara makubwa zaidi ambayo yangeweza kulitikisa taifa," amesema Dk.Migiro.

Aidha amefafanua kuwa jukumu kuu la vyombo vya ulinzi na usalama kwa Jeshi la Polisi ni kulinda raia na mali zao wakati Jeshi la Wananchi wa Tanzania jukumu lao ni kulinda mipaka ya nchi.

“Tunavipongeza vyombo vya ulinzi na usalama vilifanya kazi kubwa ya kuhakikisha nchi inakuwa salama, pamoja na kuwepo kwa dosari ndogo lakini vilifanya kazi kubwa.”

Dk.Migiro pia alitumia nafasi hiyo kukanusha madai ya kwamba vyombo hivyo hasa Jeshi la Polisi linaingia katika siasa kwa ajili ya kukilinda Chama Cha Mapinduzi ambapo alisisitiza sio kweli na kwamba vyombo hivyo ni vya Taifa na vinahudumia  Watanzania wote bila kujali tofauti zao za kisiasa.

Wakati huo huo Dk.Migiro amesema CCM inaendelea kuamini katika umuhimu wa maridhiano kama msingi wa kudumisha umoja, amani na mshikamano wa Taifa baada ya matukio yaliyotokea Oktoba 29 mwaka jana.

Ameongeza Chama hicho kinaunga mkono juhudi zote zinazolenga kuimarisha mshikamano wa Watanzania huku kikisisitiza kwamba maridhiano ni mchakato endelevu wa kujenga taifa imara lenye amani na maendeleo.

Kuhusu ripoti ya tume ya uchunguzi iliyoundwa kufuatia matukio hayo, Dk.Migiro amesema CCM iliipokea kwa umakini mkubwa kutokana na uzito wa tukio hilo ambalo halijawahi kushuhudiwa katika miaka yote nchini ambapo amesisitiza ni tukio ambalo limeitia doa nchi na limeshutua.

Amesema  chama kilichukua muda kutafakari kwa kina yaliyotokea kabla ya kutoa msimamo wake rasmi kuhusu ripoti hiyo iliyoongozwa na Jaji Chande.

Pia alipongeza kuundwa kwa tume hiyo pamoja na kazi iliyofanywa na wajumbe wake kwa weledi mkubwa huku akiwashukuru wananchi waliojitokeza kutoa ushahidi na maoni yao yaliyosaidia kukamilika kwa uchunguzi huo.

Kuhusu  vifo vilivyotajwa kwenye ripoti hiyo, Dk.Migiro amesema CCM imepokea kwa masikitiko makubwa taarifa ya vifo vya watu 518 akisisitiza kuwa hata kifo cha mtu mmoja ni pigo kubwa kwa taifa.

Amesema  chama hicho hakina sababu ya kupinga takwimu zilizotolewa na tume kwa kuwa zimetokana na taarifa kutoka hospitali, Msajili wa Vizazi na Vifo pamoja na vyanzo vingine rasmi.

Dk.Migiro pia alieleza kipindi chote cha kampeni za uchaguzi mkuu wa Oktoba mwaka jana kulikuwa na hali ya utulivu na vyama vyote vilifanya shughuli zao kwa amani kufuatia wito wa Rais na Mwenyekiti wa CCM, Dk. Samia Suluhu Hassan wa kufanya siasa za kistaarabu.





Top News