Na Oscar Assenga, Muheza
MJUMBE wa Kamati ya Hamasa Kanda ya Kaskazini wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Lukindo Mohamed, ametangaza rasmi kujiondoa ndani ya chama hicho na kueleza kuwa hatarajii kujiunga na chama kingine chochote cha siasa.

Lukindo, ambaye pia aliwahi kuwa Kaimu Katibu wa Baraza la Wazee Mkoa wa Tanga na Mjumbe wa Kamati ya Utendaji Wilaya ya Muheza, amesema amefikia uamuzi huo kwa hiari yake mwenyewe ili aweze kuwa huru na kujikita katika shughuli zake binafsi, ikiwemo kilimo na malezi ya familia.

Akizungumza na waandishi wa habari Lukindo alieleza kuwa moja ya sababu kubwa ya kujiondoa kwake ni kutoridhishwa na mwelekeo wa chama chake, hususan kuhimiza maandamano kama njia ya kutatua changamoto za kisiasa.
Alisema kuwa licha ya Tanzania kuwa nchi ya kidemokrasia inayoruhusu wananchi kuchagua viongozi kwa kura bado kumekuwa na msisitizo wa mara kwa mara wa kufanya maandamano, jambo ambalo linaweza kusababisha madhara kwa wananchi, ikiwemo majeruhi na vifo.

“Naamini kabisa kuwa suluhu ya matatizo ya nchi yetu haiwezi kupatikana kupitia maandamano, bali kupitia mazungumzo na maridhiano ni muhimu viongozi wa vyama vya siasa kukaa pamoja na kujadiliana kwa lengo la kuijenga nchi,” alisema Lukindo.

Aliongeza kuwa hajashawishiwa na mtu yeyote kuchukua uamuzi huo, bali ametumia busara na uzoefu wake wa muda mrefu katika siasa, akieleza kuwa amehudumu ndani ya chama hicho tangu mwaka 1992 katika ngazi mbalimbali, ikiwemo Katibu wa Wilaya ya Muheza kuanzia mwaka 2010 hadi 2024.

Kwa upande wake, aliyekuwa Mwenyekiti wa Chadema Wilaya ya Lushoto, Andrew Mjema, naye ametangaza kujiondoa ndani ya chama hicho, akieleza kuwa amechoshwa na kile alichokiita siasa za matamko na maandamano zisizo na tija kwa wanachama wa kawaida.

Mjema alisema kuwa mara nyingi viongozi wa juu wamekuwa wakitoa wito wa maandamano huku madhara yake yakiwakumba zaidi wanachama wa ngazi za chini, hali ambayo ameona si ya haki.

“Viongozi wanazungumza kuhusu maandamano lakini hawashiriki moja kwa moja, wanaoumia ni wanachama wa chini. Hii si sawa, ndiyo maana nimeamua kujiondoa na kuendelea na shughuli zangu za ufundi,” alisema Mjema.

Alisisitiza kuwa hatajiunga na chama chochote cha siasa, akiongeza kuwa anahitaji muda wa kujiendeleza kiuchumi na kuishi maisha yake binafsi nje ya siasa.

Wote wawili wamehitimisha kwa kushauri vyama vya siasa nchini kuweka mbele mazungumzo na maridhiano badala ya maandamano, wakiamini kuwa hiyo ndiyo njia sahihi ya kudumisha amani na kuleta maendeleo nchini.

Majiko 200,000 yameanza kusambazwall, mengine 300,000 yatasambazwa mwaka fedha wa 2026/2027

Wakala wa Nishati Vijijini (REA) umeshaanza kuwawezesha Wafanyabiashara wadogo wa chakula hususan Mama na Baba lishe ili watumie majiko bunifu.

Kundi hilo limeanza kuwezeshwa kupitia Mradi wa majiko banifu ambapo takribani majiko 200,000 ambayo yameanza kusambazwa mwaka wa fedha wa 2025/2026 kwa njia ya ruzuku ya hadi asilimia 85 ambapo imeelezwa hatua hiyo itakayopunguza kwa kiasi kikubwa gharama za nishati kwa 
Watumiaji.

Hayo yameelezwa Aprili 21, 2026 na Mhandisi Mwandamizi kutoka REA, Deusdedit Malulu wakati wa Kongamao la Kitaifa la Mama na Baba Lishe Tanzania lililoandaliwa na Umoja wa Mamalishe Tanzania (UMALITA) lililofanyika ukumbi wa Kimataifa wa mikutano Julius Nyerere, Jijini Dar es Salaam.


Mhandisi Malulu amesema REA imeendelea kuwa mstari wa mbele katika kuwawezesha Baba na Mama lishe nchini ili watumie teknolojia za nishati safi ya kupikia kupitia Miradi mbalimbali yenye lengo la kupunguza gharama na kuongeza upatikanaji wa nishati hiyo.


"Na inafanya hivyo kwa sababu miongoni mwa majukumu yake ni kuhamasisha na kuwezesha upatikanaji wa nishati zote, hususani nishati hiyo safi ya kupikia."

Amesema ushiriki wa REA katika kongamao hilo umelenga kutoa elimu na kuwafahamisha Washiriki kuhusu fursa zilizopo katika Miradi ya nishati safi, ikiwamo ruzuku ya mitungi ya gesi na majiko banifu.

“Tunayo Miradi mingi inayolenga kuhakikisha Baba lishe na Mama lishe wanapata nishati safi kwa bei nafuu na kwa wingi. Hii ni pamoja na utoaji wa ruzuku kwenye mitungi ya gesi na majiko banifu,” amesema, Mhandisi, Malulu.

Aidha ameongeza kuwa REA imeendelea kushirikiana na Wadau mbalimbali kuhakikisha teknolojia za nishati safi zinawafikia wananchi katika maeneo yote nchini.

Ameutaja pia Mradi wa Kusambaza Gesi Asilia hadi kwenye makazi ya Watu; Mradi unaoanzia Mtwara; Lindi hadi Dar es Salaam ambapo hadi sasa kaya takribani 980 zimeunganishwa na mabomba ya gesi asilia ya kupikia kwa ushirikiana na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC).

Mhandisi, Malulu amesema kuwa juhudi za kuhamasisha matumizi ya nishati safi zilianza mwaka 2021; ambapo matumizi yalikuwa kati ya asilimia mbili hadi sita na kwamba hadi sasa matumizi yameongezeka na kufikia takribani asilimia 23 hadi 25.

Amesema lengo la Serikali ni kuhakikisha ifikapo mwaka 2034, angalau asilimia 80 ya Wananchi wawe wanatumia nishati safi ya kupikia.

Amesema kasi ya utekelezaji wa miradi iliyopo inaonesha uwezekano mkubwa wa kufikia lengo hilo mapema.

“Mama lishe na baba lishe ni kundi muhimu sana katika kufanikisha azma hii. Wanapotumia nishati safi wanapunguza gharama na kuboresha mazingira ya kazi zao, hivyo tunawapa kipaumbele katika miradi yetu,” amesisitiza.

Kadhalika, Maluku ameeleza kuwa, REA itaendelea kubuni zaidi Miradi ya kibunifu ili kuwafikia wananchi wengi zaidi, hasa wale wa kipato cha chini, kwa lengo la kuhakikisha nishati safi ya kupikia inapatikana kwa urahisi na kwa bei nafuu kwa Wananchi wote.
RAIS Mstaafu Dkt. Jakaya Mrisho, yuko Boston, Marekani ambapo anashiriki kutoa mafunzo kwa Mawaziri wakiwemo wa Fedha na wa Mipango kutoka nchi mbalimbali zinazoendelea kupitia Mpango wa Uongozi wa Ngazi ya Mawaziri wa Harvard “Harvard Ministerial Leadership Program” inayoendeshwa na Chuo Kikuu cha Harvard.

Mheshimiwa Rais Mstaafu ni mmoja wa Viongozi Wakuu wa Kitaifa Wastaafu wanaoshiriki kutoa mafunzo hayo.

Pamoja na Viongozi Wakuu wa Kitaifa Wastaafu, wengine wanaoshiriki kutoa mafunzo hayo ni pamoja na Wakuu wa Taasisi za Kimataifa, Mashirika Binafsi na Wabobezi katika masuala ya sera, uchumi na maendeleo kutoka sehemu mbalimbali duniani.

Kutoka Tanzania, mafunzo hayo yamehudhuriwa na Mhe. Khamis Mussa Omar, Waziri wa Fedha; Mhe. Prof. Kitila Alexander Mkumbo, Waziri Ofisi ya Rais - Mipango na Uwekezaji; na Mhe. Juma Malik Akil, Waziri wa Fedha na Mipango wa Zanzibar.

KAMPUNI Ya ubashiri ikishirikiana na Taasisi ya Tulia trust kupitia Betika Mbeya Tulia Marathon imezindua rasmi jezi ambayo itatumika Msimu wa 10 wa Mashindano Jijini Mbeya mwaka huu.

Akizungumza na Wanahabari  Jijini Dar es Salaam Meneja Mkuu wa Betika Tanzania Samuel Mcheru amesema Betika inathamini sana michezo na itaendelea kutoa ushirikiano mkubwa kupitia Taasisi ya Tulia trust Kuhakikisha mbio hizo za Betika Mbeya Tulia Marathon zinafanyika kwa ufanisi mkubwa .

Hata hivyo ameongeza kuwa mashirikiano hayo yanalenga kuwaweka wananchi karibu na kushiriki michezo ili kuweka miili yao imara zaidi,kurudisha tabasamu kwa jamii na kutoa fursa za kibiashara kwa Wananchi wa Jiji hilo.

Mcheru ametoa wito kwa Makampuni mengine yawe yenye tija katika jamii kwani uwepo wa Betika Tulia Marathon ni kiashiria tosha kuwepo kwa ongezeko la kipato kila inapofanyika kutokana na jamii kukusanyika eneo moja hivyo inawapa fursa betika pia kujitangaza zaidi na Wafanyabiashara kuendesha shughuli zao.

Kwa upande wake Mbunge wa Mbeya na Spika wa Bunge Mstaafu Dkt.Tulia Ackson amesema Kampuni ya Betika imekuwa na mchango mkubwa wa kuhakikisha mbio hizo zinafanyika kwa ufanisi mkubwa hasa kwa mchango wao wa vifaa vya kushiriki mbio hizo pamoja na miundombinu mbalimbali pindi linapokuja shindano hilo kutokana na kuweka udhamini wao kwa zaidi ya Miaka mitatu.

Ackson amesema kwa mwaka huu shindano hilo linatimiza miaka 10 tangu kuanzishwa kwake na kwa mwaka huu wanategemea kukusanya kiasi cha fedha shilingi milioni 300 ili kugusa Maeneo ya Kijamii mbalimbali ikiwemo Kuboresha makazi ya Wahitaji, eneo la Afya hususani kujenga baadhi ya wodi hitajika, vifaa pamoja na eneo la Elimu Mashuleni.

Hata hivyo amesema Mbio hizo za kipekee zilizopewa chachu na hali ya hewa ya jiji hilo itatimua vumbi Mei 15 na 16 zikiambatana na burudani mbalimbali.

Aidha amevipongeza vyombo vya habari kwa kuendelea kutoa habari juu ya Taasisi ya hiyo ambayo kutokana na michango ya wadau mbalimbali katika kujikita kusaidia jamii.

Pia ametoa wito kwa Watanzania kujiandikisha kushiriki katika mbio hizo kupitia Ofisi zilizopo Jijini Mbeya pamoja na kujisajili mtandao kwenye kurasa za Taasisi hiyo.

Nae Afisa Habari wa Kampuni ya Betika Juvenalius Rugambwa aliongeza kuwa Jezi hiyo iliozinduliwa itatumika rasmi kwenye mbio hizo huku akisherehesha kuwa jezi hizo zimepambwa na rangi zenye mvuto zaidi zenye michoro ya vivutio vilivyopo Tanzania ikiwemo bendera ya Taifa .


 

Tanzania ni miongoni mwa nchi 10 za juu katika utoaji wa taarifa za biashara kati ya nchi 166 ambazo ziko chini ya Shirika la Biashara Duniani (WTO).

Hayo yamesemwa na na Mkurugenzi wa Sera na Mipango wa Wizara ya Viwanda na Biashara Bw. Needpeace Wambuya wakati akifungua Warsha ya kitaifa ya mafunzo kuhusu taarifa za Shirika la Biashara Duniani kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Aprili 21, 2026 katika Ofisi za Wizara jijini Dodoma.

Bw. Wambuya amesema mafunzo hayo yatasaidia kuvutia wawekezaji, kuwa na imani na taarifa, kuongeza uwazi wa taarifa na kufanya taarifa zinazopelekwa zisaidie kuondoa vikwazo vya kibiashara ambazo zimekuwa ni changamoto ya ufanyaji wa biashara duniani.

Amebainisha kuwa mafunzo hayo yamewalenga wataalam wa sekta za Serikali lakini na sekta binafsi kwa nia ya kuwajengea uwezo wataalamu wa biashara juu ya namna ya kuratibu utoaji wa taarifa aina ya taarifa za biashara zinazotolewa na wakati unaofaa kutoa taarifa.

Mafunzo hayo yanatarajiwa kufanyika kwa siku nne katika Ofisi za Wizara ya Viwanda na Biashara yakijumuisha maafisa kutoka taasisi mbalimbali za umma na binafsi.

Pamela Mollel Arusha.

Meya wa Manispaa ya Kibaha, Dk Nicas Mawazo, amejitosa katika kinyang’anyiro cha uongozi wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania, huku akiahidi kuleta mageuzi yatakayoiimarisha taasisi hiyo katika kusimamia maendeleo ya serikali za mitaa nchini.

Uchaguzi huo unatarajiwa kufanyika kesho, Aprili 22, 2026, katika Arusha International Conference Centre, ambapo Dk Mawazo anawania nafasi ya uenyekiti inayoshikiliwa kwa sasa na Murshid Hashim Ngese.

Katika kinyang’anyiro hicho, Dk Mawazo anatarajiwa kuchuana na wagombea wengine akiwemo Sima Constantine Sima pamoja na Maximilian Iranghe.

Akizungumza na waandishi wa habari Aprili 21, 2026, mara baada ya kurejesha fomu ya kuomba ridhaa, Dk Mawazo amesema dhamira yake ni kuifanya ALAT kuwa chombo imara zaidi kitakachowezesha utekelezaji bora wa miradi ya maendeleo katika sekta mbalimbali.

“Nimekuja kurejesha fomu ya uchaguzi wa ALAT ili kuomba ridhaa ya kuongoza taasisi hii muhimu kwa maendeleo ya nchi yetu,” amesema.

Ameongeza kuwa akichaguliwa, atahakikisha ALAT inaimarika zaidi ili iwe sauti ya wananchi na kurahisisha utekelezaji wa miradi ya maendeleo ikiwemo elimu, afya, barabara na huduma nyingine za kijamii.

“Sisi ndio tunaoletewa fedha na kuzielekeza kwenye miradi ya wananchi kama hospitali, shule na miundombinu ya barabara,” amesema.

Aidha, Dk Mawazo amesema licha ya mafanikio yaliyofikiwa na ALAT, bado kuna haja ya kuimarisha mifumo ya uendeshaji ili kuongeza ufanisi na matokeo chanya kwa jamii.

“ALAT ina mafanikio, lakini nikipata nafasi nitaleta mabadiliko makubwa kutokana na uzoefu wangu wa uongozi. Ninaamini naweza kuongoza taasisi hii kwa ufanisi zaidi,” ameongeza.

Mkutano huo wa uchaguzi utafunguliwa na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mwigulu Lameck Nchemba.

Kwa mujibu wa Kaimu Katibu Mkuu wa ALAT, Thomas Vungwa, mkutano huo wa siku mbili utahusisha uchaguzi wa Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti pamoja na wajumbe wa Kamati ya Utendaji.

Amesema wajumbe kutoka halmashauri 184 nchini wanatarajiwa kushiriki, huku mchakato wa uchukuaji na urejeshaji wa fomu ulioanza Aprili 17, 2026 ukifikia tamati sambamba na kuanza kwa uchaguzi huo kesho.





Babati, Manyara
KAMPUNI ya mtandao wa simu ya Airtel Tanzania imekabidhi zawadi ya bajaji mpya kwa mshindi wa kampeni ya Mwaka Umenyooka na Airtel, Bw. Barnaba Dominick, mkazi wa Wilaya ya Babati mkoani Manyara, baada ya kujishindia kupitia matumizi ya huduma ya Airtel Money.

Akizungumza katika hafla ya makabidhiano hayo, Meneja wa Airtel Kanda ya Manyara, Kephar Kileo, amesema kuwa kampeni hiyo imelenga kuwazawadia wateja wanaotumia My Airtel App kufanya miamala yao ya kila siku, huku akibainisha kuwa wateja hao wamekuwa na nafasi kubwa ya kujishindia zawadi mbalimbali.

“Tunawapongeza wateja wetu kwa kuendelea kutumia huduma za Airtel, hususan My Airtel App. Kupitia kampeni ya Mwaka Umenyooka na Airtel, tumetoa zawadi mbalimbali ikiwemo pikipiki, magari, bajaji pamoja na fedha taslimu, kama njia ya kuthamini uaminifu wao,” alisema Kileo.

Kwa upande wake mshindi wa bajaji hiyo, Bw. Barnaba Dominick, ameonesha furaha yake kwa kushinda zawadi hiyo, akieleza kuwa itamsaidia kuboresha maisha yake kwa kuongeza kipato kupitia biashara ya usafirishaji wa abiria katika maeneo ya Babati.

“Nashukuru Airtel kwa zawadi hii kubwa. Bajaji hii itanisaidia kuanzisha na kukuza biashara yangu ya usafirishaji na hivyo kuongeza kipato changu na familia yangu,” alisema Dominick.

Aidha, amewahamasisha Watanzania wengine kuendelea kutumia My Airtel App kufanya miamala mbalimbali ili kupata nafasi ya kushinda zawadi zinazotolewa na Airtel Tanzania kupitia kampeni hiyo.

Airtel Tanzania inaendelea kujizatiti katika kutoa huduma bora za mawasiliano na kifedha pamoja na kuendesha kampeni bunifu zinazolenga kuwainua wateja wake kiuchumi.

Benki ya NMB imetoa udhamini wa Sh milioni 100 kwa ajili ya kusaidia maandalizi na uendeshaji wa Mkutano Mkuu wa 40 wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT) utakaofanyika jijini Arusha. Udhamini huo unaongeza nguvu katika maandalizi ya mkutano huo muhimu unaotarajiwa kuwakutanisha wajumbe kutoka mamlaka mbalimbali za serikali za mitaa nchini.

Makabidhiano ya mfano wa hundi hiyo yalifanywa na Meneja wa NMB Kanda ya Kaskazini, Baraka Ladislaus, kwa Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya mkutano huo, Juma Hokororo, katika hafla iliyoshuhudiwa na Kaimu Katibu Mkuu wa ALAT, Thomas Vungwa. Msaada huo unalenga kuchangia kufanikisha mkutano huo wa uchaguzi pamoja na maandalizi yake kwa ujumla.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Baraka alisema NMB imeendelea kuwa mshirika wa ALAT kwa zaidi ya miaka 10, jambo linalotokana na kutambua mchango wa jumuiya hiyo katika kusukuma maendeleo kupitia serikali za mitaa.

 Alisema benki hiyo itaendelea kuunga mkono juhudi zinazosaidia kuimarisha taasisi zinazogusa maisha ya wananchi moja kwa moja.

Kwa upande wake, Hokororo aliishukuru NMB kwa mchango huo, akisema umefika kwa wakati muhimu kuelekea mkutano huo wa kitaifa. Alisema ushiriki wa wadau kama NMB unaendelea kuwa nguzo muhimu katika kufanikisha mkutano wa ALAT, ambao ni jukwaa muhimu kwa uchaguzi wa viongozi na mjadala wa masuala ya maendeleo ya serikali za mitaa.

Meneja wa benki ya NMB Kanda ya kaskazini Baraka Ladislaus (wa pili kulia) akimkabidhi mwenyekiti wa kamati ya maandalizi ya mkutano wa jumuiya ya tawala za mitaa taifa (ALAT) Juma Hokororo mfano wa hundi ya sh100 milioni waliyotoa kudhamini mkutano wa uchaguzi wa jumuiya hiyo, ikishuhudiwa na kaimu katibu mkuu wa ALAT Thomas Vungwa (wa pili kushoto) na Amanda Feruzi Meneja Mwandamizi  Biashara za Serikali Benki ya NMB.









LEO tarehe 22 Aprili 2026, Ligi Kuu ya Uingereza inatoa burudani ya kiwango cha juu kwa mashabiki wa soka, ikiwa na mechi mbili muhimu zitakazopigwa kuanzia saa 10:00 usiku. Mechi ya kwanza ni kati ya AFC Bournemouth dhidi ya Leeds United kwenye uwanja wa Vitality Stadium, na nyingine ni Burnley wakiwa wenyeji wa Manchester City kwenye uwanja wa Turf Moor.

Ratiba hii imebadilishwa kutoka wikendi ya Aprili 25 hadi wiki hii kufuatia mafanikio ya Leeds United na Manchester City kufika nusu fainali ya Kombe la FA, hivyo kuwaruhusu timu hizo kuzingatia mashindano hayo bila msongamano wa mechi wikendi ijayo. Katika mechi ya kwanza, AFC Bournemouth itakuwa mwenyeji wa Leeds United kwenye uwanja wao wa Vitality Stadium.

Leeds wanaanza mechi hii wakiwa katika hali ya kusisimua kiakili baada ya kufuzu kwa nusu fainali ya FA Cup kwa mara ya kwanza tangu 1987, lakini changamoto yao kubwa bado ni kunusurika kushuka daraja. Hata hivyo, wataikosa Bournemouth wakiwa na wachezaji wao muhimu kama Tyler Adams, Marcus Tavernier, na Justin Kluivert wote wakiwa majeruhi, wakati Leeds wana wasiwasi wa majeruhi wa kikosi kikiwemo Daniel James na Anton Stach.

Upande wa pili, Burnley wanakaribisha Manchester City kwenye uwanja wao wa Turf Moor, lakini wanaingia kwenye mechi hii wakiwa na hali mbaya ya kushuka daraja. Burnley wako pointi 20 na mechi sita tu zimesalia, hivyo kushindwa kwao kunaweza kuharakisha kushuka kwao daraja. Kocha Scott Parker amekiri kuwa timu yake inajiandaa kwa Championship, jambo ambalo linaweza kuathiri kiwango na ari ya wachezaji wake.

Ingia kwenye kasi ya kujishindia pesa kwenye michezo ya Kasino ya Mtandaoni kama vile, Keno, Aviator, Poker, Roulette, Wild Icy Fruits, Super Heli na mingine kibao. Jiunge leo kwa kutembelea tovuti ya meridianbet.co.tz au piga *149*10# kisha uanze safari yako ya ushindi.

Kwa upande mwingine, Manchester City wanaingia kwenye mchezo huu wakiwa na lengo la kushinda ubingwa, na wana nguvu kamili licha ya majeruhi kadhaa muhimu kama Ruben Dias na John Stones. City wanatarajiwa kushambulia kwa nguvu zote, hasa wakijua kwamba Burnley wana rekodi mbaya dhidi yao.

Manchester City wako katika harakati za kuwinda taji la ligi, huku Burnley wakijaribu tu kujiweka kwenye nafasi nzuri licha ya uhalisia wa kushuka daraja. Tabia za kujihami za Burnley zitakuwa mtihani mkubwa, na kuna uwezekano mkubwa wa City kufunga mabao zaidi ya matatu.

Kwa upande wa Bournemouth na Leeds, mechi hii inatarajiwa kuwa ya kusisimua zaidi na yenye matokeo yasiotabirika. Bournemouth wakiwa nyumbani wameonyesha uwezo wa kusumbua timu kubwa. Leeds wana historia ya kuwa timu ya kusisimua chini ya kocha Daniel Farke, lakini majeruhi yanaweza kuwafanya wasiwe na nguvu kamili. Leeds wanahitaji kushinda ili kujitenga na eneo la kushuka daraja, wakati Bournemouth wana nafasi ya kufikia pointi 45 za kuwahakikishia usalama. Jisajili

 Benki ya Exim Tanzania imeingia katika ushirikiano wa kimkakati na Toyota wenye lengo la kufanya umiliki wa magari kuwa rahisi zaidi na nafuu kwa Watanzania.

Kupitia ushirikiano huu, suluhisho maalum la ufadhili wa magari limeanzishwa, likiwwawezesha watu binafsi na biashara kununua magari mapya na yaliyotumika kwa gharama ndogo ya awali Pamoja na muda nafuu wa marejesho unaoweza kufikia hadi miaka sita.

Akizungumza wakati wa hafla ya utiaji Saini huo, Mkuu wa Huduma za Benki kwa Wateja Binafsi na wa Kati wa Benki ya Exim Tanzania, Andrew Lyimo, alisema ushirikiano huo unaonesha dhamira ya Benki kuendelea kutoa suluhisho bunifu na zinazomlenga mteja moja kwa moja.

“Katika Benki ya Exim Tanzania, tunalenga kufanya zaidi ya huduma za Kibenki za kawaida kwa kutoa suluhisho zinazogusa mahitaji halisi ya kila siku ya wateja wetu. Ushirikiano huu na Toyota unatupa fursa ya kurahisisha umiliki wa magari kupitia mipango nafuu ya ufadhili inayopunguza mzigo wa kifedha huku ikiunga mkono mahitaji ya usafiri binafsi na ukuaji wa biashara,” alisema Lyimo.

Kupitia mpango huu, Benki ya Exim itatoa ufadhili wa hadi asilimia 80 ya gharama kwa magari mapya na asilimia 70 kwa magari yaliyotumika, kwa viwango vya riba shindani vinavyokokotolewa kwa mfumo wa salio linalopungua. Huduma hii inapatikana kwa Shilingi za Kitanzania na Dola za Marekani, ikiwa na malipo ya awali kuanzia asilimia 20.

Kifurushi hiki cha ufadhili wa magari kimetengenezwa ili kuwahudumia wateja mbalimbali wakiwemo waajiriwa, wajasiriamali, biashara ndogo na za kati (SMEs), pamoja na makampuni yanayohitaji suluhisho la uhakika la usafiri bila kuathiri mtiririko wa fedha.

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Toyota, Meneja Mkuu William Kadiva, alisisitiza umuhimu wa ushirikiano huo katika kupanua upatikanaji wa magari yenye ubora nchini Tanzania.

“Ushirikiano wetu na Benki ya Exim Tanzania ni hatua muhimu katika kuhakikisha magari ya Toyota yanawafikia Watanzania wengi zaidi. Kwa kuunganisha ubora wa magari yetu na suluhisho nafuu za ufadhili, tunawezesha watu wengi zaidi kumiliki magari yanayotegemewa kwa matumizi ya kila siku na shughuli za kibiashara,” alisema Kadiva.

Wateja wanaweza kupata huduma hii kwa kutembelea tawi lolote la Exim Bank au showroom za Toyota (Automark) kote nchini ili kujionea chaguo zilizopo na kuanza safari ya kumiliki gari.

Ushirikiano huu unaakisi dhamira ya pamoja ya Exim Bank na Toyota ya kuchochea shughuli za kiuchumi, kuboresha usafiri, na kuunga mkono ukuaji wa biashara nchini Tanzania.

Kuhusu Exim Bank Tanzania

Ilianzishwa mwaka 1997, Exim Bank Tanzania ni mojawapo ya taasisi zinazoongoza za kifedha nchini, inayotambulika kwa ubunifu wake, suluhisho zinazomlenga mteja, na mchango mkubwa katika ukuaji wa uchumi wa Tanzania. Ikiwa na uwepo imara wa kikanda katika nchi za Comoro, Djibouti, Uganda, na Ethiopia, Exim Bank ni miongoni mwa benki chache za asili ya Tanzania zilizofanikiwa kupanua shughuli zake nje ya mipaka ya nchi.

Kupitia mtandao wake mpana wa matawi na majukwaa ya kisasa ya huduma za benki kidijitali, Exim Bank inaendelea kuwawezesha watu binafsi na biashara kwa huduma za kifedha zilizo thabiti, rahisi kubadilika, na zenye mwelekeo wa maendeleo ya baadaye.


Kuhusu Toyota Tanzania

Toyota Tanzania Ltd, iliyoanzishwa mwaka 1965, ni msambazaji pekee wa magari ya Toyota nchini Tanzania na mdau mkuu katika sekta ya magari. Kampuni hii hutoa aina mbalimbali za magari na huduma. Imeendelea kushikilia nafasi ya uongozi katika soko la magari mapya nchini, kwa kuzingatia uendelevu na kutoa suluhisho bora za usafiri kwa wateja wake.

Mkuu wa Kitengo cha Wateja Binafsi na wa Kati wa Benki ya Exim Tanzania, Bw.Andrew Lyimo( wa pili kushoto) na Meneja Mkuu wa Toyota Tanzania Bw.William Kadiva (wa pili kulia) wakisaini mkataba wa makubaliano ya ushirikiano unaolenga kuwawezesha wateja wake kumiliki gari ya ndoto yake. Hafla hii ilifanyika ofisi za Toyota Tanzania, jijini Dar es Salaam tarehe 21 April 2026, Ikishuhudiwa na Afisa Mkuu wa Masoko na Mawasiliano wa Benki ya Exim Tanzania Bw. Stanley Kafu (kushoto) na Mkuu wa Kitengo cha Usimamizi wa Sheria wa Toyota Tanzania Bi. Lucia Minde (kulia).

▪️ Serikali, Chemba ya Migodi Wapanga Mkakati Kabambe Kukuza Uchumi Kupitia Madini

▪️ Waziri Mavunde Asikiliza na Kutatua Changamoto, Maboresho na Kuahidi Kuyafanyia Kazi

▪️ Atoa Onyo Kali kwa wamiliki wa Leseni ambao hawaziendelezi

▪️ Utafiti wa Madini Watajwa Kuwa Injini ya Uchumi wa Madini Kuelekea Uchumi wa Dola Trilioni



Serikali kupitia Wizara ya Madini kwa kushirikiana na Chemba ya Migodi Tanzania (TCM) imejadili na kuweka mikakati wa kuifanya Sekta ya Madini kuwa mhimili mkuu wa kufikia Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 ya kuifanya Tanzania kufikia uchumi wa thamani ya dola trilioni moja ifikapo mwaka 2050, kwa kusisitiza utafiti wa madini, usimamizi madhubuti na ushirikiano na sekta binafsi kama nguzo kuu za mafanikio hayo.

Akizungumza katika kikao na Chemba ya Migodi kilichofanyika katika ukumbi wa Tume ya Madini jijini Dodoma, leo Aprili 21, 2026, Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde amesema kuwa hatua hiyo haiwezekani bila kuwekeza kwa nguvu katika utafiti wa kina wa rasilimali madini kwa kushirikiana na sekta binafsi.

Ameeleza kuwa utafiti wa madini unapaswa kupewa kipaumbele kwani ndio unaofungua milango ya uwekezaji, kuongeza tija na kuhakikisha nchi inanufaika ipasavyo na rasilimali zake.

Katika kikao hicho, Waziri Mavunde amepokea changamoto, maoni na mapendekezo kutoka kwa wadau wa Sekta ya Madini kupitia TCM, akiahidi kuwa Serikali itayafanyia kazi kwa lengo la kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa wanachama wa TCM kupitisha hoja zao kupitia umoja wao ili kuwa na sauti moja yenye nguvu na kurahisisha mawasiliano kati ya Serikali na sekta binafsi.

Kwa upande wa usimamizi, Waziri Mavunde ameelekeza kuimarishwa kwa ushirikiano kati ya Ofisi ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini na taasisi za kiserikali ili kuhakikisha utekelezaji wa Sera na Sheria unakuwa na ufanisi zaidi bila kuingilia na kuleta usumbufu kwa wawekezaji.

Akizungumzia changamoto ya uvamizi wa maeneo yenye leseni halali za uchimbaji, Mavunde amesisitiza kuwa vitendo hivyo havitavumiliwa na tayari maelekezo yametolewa kwa Maafisa Madini Wakazi wa Mikoa, kupitia Ofisi ya Mtendaji Mkuu wa Tume ya Madini, kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama kuwaondoa mara moja wavamizi wote na ametumia nafasi kueleza msimamo wa serikali wa kufuta leseni ambazo hazifanyi kazi zinazomilikiwa na wawekezaji hao.

Amefafanua kuwa Serikali imeanzisha mfumo wa kidijitali unaohakikisha kuwa leseni za utafiti zinazoisha muda wake zinarejeshwa moja kwa moja Serikalini, hatua inayolenga kudhibiti tabia ya watu kushikilia maeneo makubwa kwa matarajio ya kuvutia wawekezaji baadaye.

Katika kuimarisha ajenda ya Ushirikiwa wa Watanzania kwenye sekta ya madini, Waziri Mavunde ameeleza kuwa, kuanzishwa kwa maeneo maalum ya uwekezaji wa viwanda vinavyozalisha vifaa na vipuri vya migodini, akitaja eneo la mgodi wa uliofungwa wa Buzwagi kama kitovu kinachoweza kuendelezwa kuwa ukanda maalum wa uchumi kwa shughuli hizo.

Pia, amekazia kuwa orodha ya bidhaa na huduma 20 zilizotengwa kwa Watanzania pekee katika migodi itaendelea kulindwa bila mabadiliko, akibainisha kuwa Serikali inalenga kulinda maslahi ya wazawa kwa kuzingatia sheria zilizopo.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Madini Steven Kiruswa amesema kuwa pamoja na juhudi za kuvutia wawekezaji, Serikali inaweka mkazo katika madini muhimu na ya kimkakati ambayo yanaendelea kuwa na soko kubwa katika zama za mabadiliko ya teknolojia na mazingira duniani.

Naye, Katibu Mkuu wa TCM, Eng. Benjamin Mchwampaka, ameipongeza Serikali kwa hatua zake za kushughulikia changamoto za sekta hiyo na kudumisha ushirikiano thabiti na sekta binafsi, ameongeza kuwa Serikali inashauriwa kudumisha uthabiti wa Sera, Sheria na moiongozo ya Sekta ya Madini, kwani mabadiliko ya mara kwa mara kwani huchelewesha maamuzi ya uwekezaji na kwamba mazingira ya kisheria yanayotabirika yanaongeza ushindani wa nchi, huvutia uwekezaji wa muda mrefu, na kuhakikisha rasilimali za madini zinachangia kikamilifu ukuaji endelevu wa uchumi.

Kwa upande wa Serikali, Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini Eng. Yahya Samamba amebainisha kuwa mpango maalum unaandaliwa kufadhili wataalamu wa Kitanzania kujifunza katika fani za kisasa kama uchumi wa madini (Mineral Economy), ili kuendana na mahitaji pamoja na mabadiliko ya kimataifa na kuongeza ushindani wa nchi.

Kwa ujumla, kikao hicho kimeonesha dhamira ya dhati ya Serikali na wadau wa Sekta ya Madini kujenga msingi imara utakaowezesha sekta hiyo kuwa moja ya injini ya uchumi wa Tanzania kuelekea 2050.








Na Oscar Assenga, Tanga



Kwa muda mrefu, gharama za pango zimekuwa mzigo usioonekana lakini mzito kwa taasisi nyingi nchini.

Ni gharama ambazo zimezoeleka kiasi cha kukubalika kama sehemu ya kawaida ya uendeshaji, bila kuhojiwa kwa kina iwapo zinaweza kubadilishwa kuwa fursa.

Ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Tanga, hali hiyo inaanza kuchukua mwelekeo mpya.

Fedha ambazo zilikuwa zikitumika kila mwaka kugharamia makazi ya watumishi sasa zinaelekezwa kwenye mkakati wenye dira tofauti ujenzi wa nyumba za watumishi katika kila wilaya ya mkoa.

Haya ni mabadiliko kutoka matumizi ya muda mfupi kwenda uwekezaji wa muda mrefu.





Upepo Mpya wa Ubunifu

Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Tanga, Rajab Abdurhaman, anauelezea mkakati huo kama hatua ya kimkakati inayolenga kupunguza matumizi yasiyo ya lazima na kuimarisha uwezo wa chama kuwekeza katika maendeleo mengine.

Akizungumza wakati wa ziara ya kukagua miradi ya chama mkoani humo, ikiwemo ujenzi wa nyumba za watumishi, Abdurhaman alionesha kuridhishwa na hatua nyumba hizo zilizofikiwa katika maeneo mbalimbali mkoani humo , lakini zaidi akisisitiza thamani ya mshikamano uliowezesha mafanikio hayo.

“Kwa ujumla mmefanya kazi kubwa sana. Nawashukuru wadau wote walioshiriki, kwa sababu walichotoa si msaada tu, bali ni uwekezaji ambao utaendelea kuzaa matunda,” alisema kwa msisitizo.

Kauli hiyo inaakisi mwelekeo mpya wa fikra kutazama rasilimali si kama matumizi ya papo kwa papo, bali kama uwekezaji wa muda mrefu.


Kutoka Pango kwenda Uwekezaji

Kabla ya mradi huu kuanza, baadhi ya watumishi walikuwa wakilipa hadi shilingi 200,000 kwa mwezi kama pango, huku wengine wakilipa zaidi kulingana na eneo.

Kwa mwaka mmoja, gharama hizo zilijikusanya na kuwa mzigo mkubwa kwa chama—fedha ambazo, kwa mtazamo wa sasa, zingeelekezwa kwenye miradi mingine ya maendeleo.

Sasa picha inaanza kubadilika.

Kwa makadirio ya haraka, kukamilika kwa nyumba hizo katika wilaya zote za Mkoa wa Tanga kunatarajiwa kuiwezesha CCM kuokoa hadi shilingi milioni 90 kwa mwaka.

Fedha hizo, kwa mujibu wa uongozi wa chama, sasa zinageuka kuwa mtaji mpya wa maendeleo ya ndani.

“Fedha hizi zitasaidia kufanya shughuli nyingine za maendeleo ndani ya chama. Huu ni ubunifu ambao umehimizwa na Mwenyekiti wa CCM Taifa pamoja na Kamati Kuu,” alieleza Abdurhaman.

Zaidi ya Takwimu: Ustawi wa Mtumishi

Licha ya faida za kifedha, mchango mkubwa zaidi wa mradi huu upo katika kuboresha ustawi wa watumishi.

Makazi bora, salama na yenye hadhi yanatarajiwa kuongeza ari, utulivu na ufanisi kazini—ambapo matokeo yake yanaonekana moja kwa moja katika utendaji wa kila siku.

Kwa lugha rahisi, mtumishi mwenye uhakika wa makazi ni mtumishi mwenye uhakika wa kazi bora.
Nidhamu ya Mali na Usimamizi wa Ardhi

Katika hatua nyingine, Abdurhaman alisisitiza umuhimu wa kulinda mali za chama kwa kuhakikisha maeneo yote yana hati miliki halali.

Alibainisha kuwa hatua hiyo ni muhimu katika kuzuia migogoro ya ardhi na kulinda uwekezaji wa muda mrefu wa chama.

Aidha, alihimiza upandaji wa miti ya kivuli na matunda katika maeneo ya chama, hatua inayolenga si tu kuboresha mazingira bali pia kuongeza thamani ya maeneo hayo na kulinda mipaka yake.






Wajibu wa Viongozi wa Wilaya

Viongozi wa chama katika ngazi ya wilaya wamepewa jukumu la kuhakikisha sheria za ardhi zinazingatiwa kikamilifu, ikiwemo ulipaji wa kodi ya pango la ardhi na kufuata taratibu zote za umiliki.

Hii inaweka msisitizo kwenye uwajibikaji na nidhamu ya matumizi ya mali za umma na za chama.



Hitimisho: Gharama Zinapogeuka Fursa

Kwa ujumla, mkakati wa ujenzi wa nyumba za watumishi unaibuka kama mfano wa namna taasisi zinavyoweza kubadili changamoto kuwa fursa za kiuchumi na kijamii.

Ndani ya CCM Tanga, hatua hii si tu inaboresha maisha ya watumishi, bali pia inaweka msingi imara wa uendelevu wa kifedha na kiutendaji wa chama kwa siku zijazo.

Na zaidi ya yote, inaonesha kwamba maendeleo si suala la kuongeza matumizi—bali ni sanaa ya kuyabadilisha kuwa uwekezaji.

0714543839
Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA), leo 21 Aprili 2026, imetumia fursa ya Wiki ya Nishati kuwahamasisha waheshimiwa wabunge kuwekeza katika ujenzi wa vituo vya mafuta maeneo ya vijijini pamoja na vituo vya CNG ili kuendelea kusogeza huduma kwa wananchi.

Kaimu Meneja wa Mawasiliano na Uhusiano wa EWURA, Bw. Wilfred Mwakalosi, alisema kuwa EWURA inatumia maonesho hayo kutoa elimu kuhusu namna inavyohakikisha upatikanaji wa huduma za nishati na maji kwa wakati na kwa gharama nafuu.

Alibainisha kuwa wabunge ni wawakilishi wa wananchi, hivyo kuwajengea uelewa kuhusu udhibiti, fursa za uwekezaji na utaratibu wa kupokea na kushughulikia migogoro na malalamiko kutawawezesha kuwasilisha taarifa sahihi kwa wananchi kuhusu juhudi za Serikali katika kuhakikisha upatikanaji wa huduma bora za umeme, mafuta na gesi asilia.

Akizungumza katika maonesho hayo, Ofisa Mwandamizi wa Kitengo cha Mafuta, Mha. Ibrahim Kajugusi, alisema elimu inayotolewa pia inalenga kuwafahamisha wananchi jinsi EWURA inavyosimamia upatikanaji wa huduma za mafuta nchini kwa kuzingatia ubora uliopitishwa na gharama sahihi. Aidha, aliwahamasisha wananchi kuchangamkia fursa za uwekezaji katika sekta hiyo, hususan ujenzi wa vituo vya mafuta vya gharama nafuu vijijini na mijini pamoja vituo vya kujazia gesi asilia kwenye magari (CNG).

Kwa upande wake, Bi. Achilana Mtingele, mchumi wa EWURA, alisema elimu inayotolewa imejikita katika kueleza namna EWURA inavyosimamia upangaji wa viwango vya bei za huduma za umeme, mafuta na gesi asilia. Aliongeza kuwa mamlaka hiyo huweka mizania kati ya maslahi ya watoa huduma na watumiaji, na kwamba wabunge waliopata elimu hiyo wataweza kuiwasilisha ipasavyo kwa wananchi katika maeneo yao.

Akizungumzia sekta ya gesi asilia, Mhandisi Mwandamizi wa Gesi Asilia, Mha. Evaline Rweikiza, alisema EWURA itaendelea kusimamia ubora wa miundombinu ya gesi asilia nchini na kuhamasisha matumizi yake, hususan katika magari. Alibainisha kuwa hadi sasa vituo 18 vimepata leseni ya EWURA kutoa huduma ya gesi asilia, huku vituo sita vingine vikiwa katika hatua za mwisho za kupata leseni katika mikoa ya Dar es Salaam na Pwani. Aidha, mipango inaendelea kwa baadhi ya makampuni kusambaza gesi asilia iliyokandamizwa katika mikoa ya Morogoro na Dodoma.

Kwa upande wa sekta ya umeme, Mhandisi Mwandamizi wa Umeme, Lulu Chilumba, aliwahamasisha wabunge na wadau wanaotembelea maonesho hayo kutumia mafundi umeme wenye leseni kutoka EWURA ili kuhakikisha usalama wa nyumba na mali zao. Alisema EWURA inaendelea kutoa leseni kwa mafundi umeme wenye sifa stahiki, ambapo zaidi ya leseni 1,000 zilitolewa katika mwaka wa fedha uliopita.

Naye Ofisa Rasilimali Watu Mkuu, Bi. Limi Kahabi, alisema EWURA ni mwajiri anayezingatia misingi ya usawa na haki katika mchakato wa ajira, akisisitiza kuwa taasisi hiyo huajiri kwa kuzingatia sifa, weledi na usawa kwa wote.


Watu kadhaa wamefariki dunia na wengine kujeruhiwa baada ya basi la abiria kugongana uso kwa uso na lori katika eneo la Mlima “S”, kijiji cha Lumango, wilayani Kilosa mkoani Morogoro.

Ajali hiyo ilihusisha basi la kampuni ya ZL Super Safari lililokuwa likitoka Ifakara kuelekea Morogoro, pamoja na lori lililokuwa limebeba kokoto.

Kwa mujibu wa mashuhuda wa tukio hilo, chanzo cha ajali kinadaiwa kuwa ni uzembe wa dereva wa lori aliyekuwa akijaribu bajaji iliyokuwa mbele yake, hali iliyosababisha kugongana na basi hilo.

Juhudi za kumpata Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro ili kuzungumzia tukio hilo zinaendelea.

Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Ndg. Asha-Rose Migiro, leo tarehe 21 Aprili 2026 amekutana na kufanya mazungumzo na ujumbe wa Mtandao wa Viongozi Wanawake wa Afrika (African Women Leaders Network - AWLN), ulioongozwa na Marais wastaafu wa Jamhuri ya Liberia, Mhe. Ellen Johnson Sirleaf, na Jamhuri ya Shirikisho la Kidemokrasia ya Ethiopia, Mhe. Sahle-Work Zewde, jijini Dar es Salaam.

Mazungumzo hayo yalijikita katika hali ya kisiasa nchini pamoja na matukio ya wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025, yakihusisha pia umuhimu wa kudumisha amani, utulivu na mshikamano wa kitaifa.

Ujumbe huo upo nchini Tanzania kwa ziara ya kikazi yenye lengo la kufanya mashauriano na viongozi mbalimbali wa kitaifa kuhusu maendeleo ya kisiasa na juhudi zinazoendelea za kuimarisha demokrasia na utawala bora, ikiwa ni sehemu ya mchango wa wanawake viongozi wa Afrika katika kulinda amani na utulivu barani.






Top News