Asema nchi ina usalama mkubwa wa mafuta hivyo wananchi waendelee kupata huduma muda wote

Timu maalum kuundwa kufuatilia uingizaji wa mafuta nchini


WAZIRI wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi ameitaka Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) kuhakikisha kuwa, hakuna mfanyabiashara anayeficha mafuta kwa kisingizio cha kusubiri bei za mafuta zipande kutokana na mgogoro unaoendelea katika eneo la Mashariki ya Kati ambao umepelekea baadhi ya nchi kukumbana na changamoto za upatikanaji wa mafuta.

Akizungumza jijini Dodoma katika kikao na Taasisi za Wizara zinazosimamia Sekta ya Mafuta, Mhe. Ndejembi ameeleza kuwa nchi ina usalama mkubwa wa mafuta na kwamba Serikali imejipanga vizuri kuhakikisha wananchi katika maeneo yote wanapata huduma bila vikwazo hivyo EWURA anapaswa kuhakikisha hakuna mafuta yanayofichwa katika maghala ya kuhifadhi Mafuta.

Aidha, ili kuhakikisha mafuta yote yaliyoagizwa nje ya nchi yanafika nchini kwa mujibu wa mkataba, Mhe. Ndejembi ameelekeza kuundwa kwa timu maalum kufuatilia mwenendo wa uingizaji wa Mafuta nchini ambayo itahusisha Wataalam kutoka Wakala wa Uagizaji wa Mafuta kwa Pamoja (PBPA), EWURA, Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) pamoja na Ulinzi na Usalama.

" Timu hii itakuwa na jukumu la kufuatilia hatua kwa hatua na kuhakikisha kuwa mafuta yote yaliyoagizwa ambayo yako njiani kuja nchini yanafika kwa wakati bila kikwazo wala changamoto yoyote. Hali ya biashara ya mafuta huko duniani si ya kuridhisha, baadhi ya nchi bei ya mafuta imepanda maradufu na wafanyabiashara wengine wanaweza kuingia tamaa na kupeleka mafuta huko, katika hili sitarajii kuona mikataba tuliyoingia na waagizaji wa mafuta ikikiukwa." Amesisitiza Mhe. Ndejembi

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi Asilia, Dkt. James Mataragio, amewahakikishia Watanzania kuwa nchi ina akiba ya kutosha ya mafuta hadi mwezi Julai 2026.

Amesema Serikali ilichukua hatua za mapema kwa kushirikiana na taasisi zake, ili kuhakikisha kunakuwa na uhakika wa upatikanaji wa mafuta na kwa gharama himilivu.

Ameongeza kuwa Wizara itaendelea kusimamia Taasisi zake ili kuhakikisha mafuta yaliyopo njiani yanafika kwa wakati, pamoja na kuwadhibiti wauzaji ili wasitumie changamoto iliyopo kama fursa ya kupandisha bei.

Awali, Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Uagizaji wa Mafuta kwa Pamoja (PBPA) Bw. Erasto Simon alieleza kuwa hali ya upatikanaji wa mafuta nchini iko salama ambapo ameeleza kuwa ukijumuisha mafuta yaliyopo nchini na yaliyopo njiani kuna petroli lita milioni 474 inayotosheleza siku 78, dizeli lita milioni 392 inayotosheleza siku 50 pamoja na lita milioni 55 za mafuta ya ndege zinazotosheleza siku 91.

Naye, Mkurugenzi Mtendaji Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) Bw.Mussa Makame ameeleza kuwa kuna mafuta ya kutosha ndani ya nchi na ambayo yako safarini kwani Serikali ilishasaini mikataba na wazabuni mapema kwa ajili ya uingizaji wa mafuta.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa EWURA, Dkt. James Andilile ameeleza kuwa kwa sasa soko liko sawa hakuna mfumuko wa bei hivyo EWURA itahakikisha watu hawafichi mafuta kusubiri mfumuko wa bei katika soko la dunia.

Amesema EWURA imeendela kushirikiana na wadau wa mafuta wakiwemo waagizaji na wauzaji ili kuhakikisha kama kuna changamoto zozote zinatatuliwa kwa haraka ili wananchi wapate huduma kwa uhakika.



Ikulu Zanzibar | 23 Machi 2026
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amekutana na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL), Ndugu David Nchimbi, aliyeambatana na Mkurugenzi Mkuu wa TTCL, CPA Moremi Marwa, pamoja na ujumbe wao, waliofika kujitambulisha.

Rais Dkt. Mwinyi ameahidi kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kushirikiana na TTCL katika kuimarisha mawasiliano Zanzibar kupitia huduma mbalimbali zinazotolewa na Shirika hilo.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya TTCL, Ndugu David Nchimbi, amemshukuru Rais Dkt. Mwinyi kwa ushirikiano unaoendelea kati ya Shirika hilo na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha huduma za mawasiliano nchini.

Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Dkt. Jim Yonazi amekutana na kufanya mazungumzo na Mkurugenzi Mtendaji mpya wa Tume ya Kudhibiti UKIMWI Tanzania (TACAIDS) Dkt. Adam Joseph Mrisho ambaye amefika kujitambulisha baada ya kuteuliwa na Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Kikao hicho kimefanyika tarehe 23 Machi, 2026 katika Ofisi ya Waziri Mkuu iliyopo mtaa wa Reli jijini Dodoma na kudhuriwa na Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) Dkt. James Kilabuko pamoja na Mratibu wa Masuala ya UKIMWI Bi. Adela Mpina.

Dkt.Yonazi ameahidi kumpa ushirikiano katika utekelezaji wa majukumu yake ya kila siku. (PICHA ZOTE NA OFISI YA WAZIRI MKUU).











Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeweka wazi kuwa itaendelea kushirikiana na Austria katika kuimarisha mahusiano ya kidiplomasia yanayolenga kuleta tija ya kiuchumi na usalama wa jamii.

Hayo yameelezwa Machi 23, 2026, jijini Dar es Salaam wakati wa mazungumzo kati ya Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani, Mhe. Ayoub Mahmoud (Mb), na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Austria anayeshughulikia masuala ya kisiasa, Mhe. Balozi Dkt. Hannah Liko.

Mazungumzo hayo yalijikita katika kuainisha vipaumbele vya Tanzania ndani ya Mkakati mpya wa Austria kwa Afrika (2026–2029), mkakati ambao unasisitiza ushirikiano wa usawa, ulinzi wa haki za binadamu, na utawala wa sheria kama nguzo kuu za kuelekea maendeleo endelevu.

Kuelekea utekelezaji wa mkakati huo, Mhe. Mahmoud amewasilisha vipaumbele vya Wizara vinavyolenga kuimarisha usalama na uwezo wa kukabiliana na majanga, huku mkazo mkubwa ukiwekwa katika kupambana na uhamiaji haramu, biashara haramu ya binadamu, matumizi ya dawa za kulevya, pamoja na kuzuia uhalifu wa kimtandao ambao umekuwa tishio la kimataifa.

Mhe. Mahmoud amezungumzia mfumo wa Triple-Win, unaolenga kudhibiti uhamiaji haramu huku ukifungua milango ya kisheria kwa vijana wa Kitanzania wenye ujuzi kupata ajira na mafunzo ya ufundi stadi nchini Austria, hatua inayotarajiwa kuwa suluhisho la kudumu katika kuwapatia vijana fursa za kimataifa na kupunguza utegemezi.

Aidha, Tanzania imekaribisha nia ya Austria kuwekeza katika miradi ya nishati safi na uchumi wa kijani kupitia makampuni yake, ili kusaidia mapambano dhidi ya mabadiliko ya tabianchi kupitia miradi ya pamoja ya kitafiti na kiteknolojia.

Kwa upande wake, Dkt. Liko amethibitisha utayari wa Austria kuunga mkono operesheni za kikanda za kulinda amani za Umoja wa Mataifa na kuongeza kuwa Austria itaendelea kuwa mshirika wa kimkakati katika kukuza viwanda, sayansi, na utamaduni ili kuhakikisha Tanzania inabaki kuwa mazingira salama kwa raia, uwekezaji, na utalii kwa manufaa ya mataifa yote mawili.

Vilevile amesema kupitia Shirika la Maendeleo la Austria (ADA), nchi hiyo imeahidi kuendelea kuwa mshirika wa kimkakati wa Tanzania katika kukuza utamaduni, sayansi, na maendeleo ya kijamii.












Benki ya NMB imetwaa tuzo tatu katika Tuzo za Euromoney Private Banking 2026 jijini London, ikishinda Benki Bora ya Huduma za Wateja Maalum Tanzania, Benki Salama Zaidi ya Huduma za Wateja Maalum na Benki Bora kwa Uendelevu Tanzania.

Ushindi huo unazidi kuakisi uimara wa benki ya NMB yenye matawi 241 nchini na zaidi ya mawakala 73,000 pamoja na  wateja zaidi ya 9.9 millioni, katika kutoa huduma mahususi kwa wateja, kuimarisha usalama wa fedha na kuongoza katika utekelezaji wa mikakati ya fedha endelevu. 

Mafanikio haya yanaendelea kuimarisha nafasi ya Benki ya NMB kama kinara wa ubunifu na mshirika wa maendeleo ya uchumi Tanzania.




SERIKALI imetangaza mpango wa kuongeza ndege nane kwa Shirika la Ndege Tanzania (ATCL), hatua itakayofikisha jumla ya ndege 24 ifikapo mwaka 2030, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha usafiri wa anga na kuchochea ukuaji wa uchumi wa Taifa.

Taarifa hiyo imetolewa na Naibu Waziri wa Uchukuzi, David Kihenzile, kwa niaba ya Waziri wa Uchukuzi, alipokuwa akizungumza na watumishi wa ATCL katika miji ya Cape Town na Johannesburg nchini Afrika Kusini, ambapo ameelezea kuwa shirika hilo lilianza na ndege moja mwaka 2016 na sasa lina ndege 16

Aidha, katika kipindi cha miaka minne ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan, serikali imeongeza ndege sita kubwa, kwa lengo la muda mfupi ni kufikia ndege 19 ndani ya mwaka wa fedha 2025/2026, kabla ya kufikia ndege 24 ifikapo mwaka 2030.

Ongezeko hilo la ndege limewezesha kupanuka kwa mtandao wa safari za ndani, ambapo kwa sasa ATCL inahudumia miji mbalimbali ikiwemo Dar es Salaam, Dodoma, Mwanza, Kilimanjaro, Arusha, Mbeya, Mtwara, Kigoma, Iringa, Pemba, Unguja, Songea, Mpanda, Tabora na Bukoba. Aidha, mipango ipo ya kuanza safari katika miji ya Sumbawanga, Musoma na Shinyanga hivi karibuni.

Katika ngazi ya kimataifa na kikanda, shirika hilo linaendesha safari zake katika miji ya Nairobi, Entebbe, Bujumbura, Lubumbashi, Lusaka, Harare, Johannesburg, Guangzhou (China), Mumbai (India) na Dubai, pamoja na huduma za usafirishaji mizigo (cargo) zinazochangia kukuza biashara na uchumi wa taifa.

Katika hotuba yake, Kihenzile amewahimiza watumishi wa ATCL kuendelea kufanya kazi kwa weledi, nidhamu na uwajibikaji kwa manufaa ya taifa.

Kwa upande wake, Balozi wa Tanzania nchini Afrika Kusini, James Bwana, amebainisha kuwa uwepo wa ATCL katika miji ya Johannesburg na Cape Town unachochea ukuaji wa biashara kati ya Tanzania na Afrika Kusini.





NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

TAASISI ya Help to Help East Africa imeendesha mafunzo ya siku 14 kwa wasichana 150 kutoka mikoa 20 nchini, ikiwa na lengo la kuwawezesha kupata ujuzi wa matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ili kuongeza ushindani wao katika soko la ajira.

Mafunzo hayo yanawalenga zaidi wasichana waliopo vyuoni pamoja na waliohitimu masomo yao, ili kuwajengea uwezo wa kitaalamu unaohitajika katika ajira za kisasa.

Tangu kuanzishwa kwa mradi huo mwaka 2015, tayari umewafikia takribani vijana 11,000 nchini, wakiwemo wanafunzi wa vyuo na wahitimu.

Akizungumza katika mafunzo hayo, Meneja wa Mradi wa taasisi hiyo, Epifania Muhagama, amesema mradi huo unalenga kuwasaidia wasichana wasio na ujuzi wa awali wa TEHAMA kwa kuwapatia maarifa muhimu kama uandishi wa ripoti, uchambuzi wa data, matumizi ya barua pepe, akili mnemba (AI), pamoja na matumizi ya kompyuta kwa ujumla.

Amesema tafiti zinaonesha kuwa ushiriki wa wanawake katika soko la ajira bado uko chini, hali inayochangiwa na kukosa kujiamini pamoja na ukosefu wa ujuzi unaohitajika.

“Mradi huu umeanzishwa baada ya tafiti kubaini kuwa wanawake wengi hawajiamini na hawana ujuzi wa kuwasaidia kupata ajira,” amesema Muhagama.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Uendelezaji TEHAMA kutoka Tume ya TEHAMA na Tafiti iliyo chini ya Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Bw. Gerson Ndanguzi, amesema mafunzo hayo ni muhimu katika kuwajengea wanawake fursa za kidijitali na kusaidia maendeleo ya familia na jamii kwa ujumla.

Ameongeza kuwa ujuzi huo unalenga kuwasaidia washiriki kutumia TEHAMA kwa usahihi kwa ajili ya maendeleo endelevu ya kiuchumi.

Aidha, Ndanguzi amewahimiza wadau mbalimbali kujitokeza kusaidia kutoa mafunzo ya TEHAMA kwa watu wengi zaidi, akibainisha kuwa bado kuna idadi kubwa ya wananchi ambao hawajafikiwa.

Pia amewasisitiza washiriki kuendelea kujifunza zaidi hata baada ya mafunzo hayo, badala ya kuridhika na ujuzi walioupata pekee.

Naye mnufaika wa mafunzo hayo, Shalom Kokonyo, amesema anatarajia kujifunza ujuzi wa kompyuta, uongozi pamoja na uwekezaji ili kuleta mabadiliko chanya katika jamii yake.

Mafunzo hayo yanatarajiwa kufanyika kwa siku 14, yakihitimishwa Aprili 1, 2026, ambapo wataalamu kutoka kada mbalimbali za ajira watashiriki kama wazungumzaji. 






















Top News