Mwezi Aprili 2026 unabaki kuwa kipindi kinachoakisi uongozi wa vitendo uongozi unaosikiliza, unaouliza maswali sahihi na unaotafuta majibu yenye tija kwa wananchi, ni mwezi ambao umeonesha kwa dhahiri namna Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Dodoma, Dkt. Neema Peter Majule, anavyobeba dhamana ya uwakilishi kwa uzito na weledi.

Ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Majule ameendelea kuwa sauti ya wale wanaotazama matumaini yao kupitia viongozi wanawake, vijana na watu wenye ulemavu, Kwa hoja zenye mwelekeo wa maendeleo, alihoji ni lini Serikali itawekeza kikamilifu katika ujenzi wa viwanda vitakavyofungua milango ya ajira, akisisitiza kuwa mikopo midogo midogo, ingawa ni muhimu, haiwezi peke yake kubadili kwa kiwango kikubwa maisha ya watu.

Majibu ya Serikali yalieleza mwelekeo wa hatua kwa hatua kuwa baadhi ya wanufaika wa mikopo hiyo wameweza kukuza biashara zao, kurejesha mikopo na hatimaye kufikia hatua ya kupata mitaji mikubwa iliyowezesha kuanzishwa kwa viwanda vidogo, hii ni picha ya mafanikio yanayokua taratibu, lakini pia inaacha nafasi ya kujiuliza: je, kasi inaweza kuongezwa zaidi?

Katika kuonesha kuwa uongozi si kauli pekee bali ni matokeo yanayoonekana, tarehe 14 Aprili 2026, Dkt. Majule aliratibu utoaji wa mikopo ya shilingi bilioni moja kwa wanawake na vijana wajasiriamali wa Mkoa wa Dodoma kwa kushirikiana na Benki ya CRDB, Hapa ndipo nadharia inakutana na uhalisia ndoto za wajasiriamali zikipewa mtaji, na juhudi zao kupewa mwelekeo mpya wa ukuaji.

Kwenye sekta ya miundombinu, alielekeza mjadala kwenye changamoto ya mvua zinazosababisha uharibifu wa barabara Dodoma, kwa mtazamo wa mbele, aliitaka Serikali kuweka mifumo ya kudumu ya mifereji ili kulinda uwekezaji huo muhimu.

Serikali ilijibu kwa kueleza kuwa inaboresha usanifu wa barabara zote mpya ili ziwe na mifereji ya kudumu ya maji, hatua inayolenga kuongeza uimara na maisha ya miundombinu hiyo, hii inaonesha jinsi hoja zinavyoweza kuwa chachu ya maboresho ya sera na utekelezaji.

Aidha, alifuatilia kwa karibu ujenzi wa barabara ya Kongwa Junction hadi Mpwapwa na Kibakwe ni barabara ambayo kwa muda mrefu imekuwa kilio cha wananchi, swali lake lilikuwa la moja kwa moja ni lini barabara hiyo itajengwa kwa kiwango cha lami?

Majibu ya Serikali yalieleza kuwa utekelezaji wake utategemea vipaumbele vilivyopo, huku miradi yenye mikataba tayari ikipewa kipaumbele. Ni jibu linaloonesha uhalisia wa upangaji wa miradi ya kitaifa, lakini pia linatoa mwanga wa matarajio ya utekelezaji wake hapo baadaye.

Katika eneo la haki na ustawi wa jamii, tarehe 24 Aprili 2026, Dkt. Majule aligusa moyo wa wengi kwa kuzungumzia ucheleweshaji wa vyeti vya vifo kutoka RITA, Hapa hakuzungumza kwa takwimu pekee bali kwa uhalisia wa maisha ya yatima wanaokwama kielimu na wajane wanaochelewa kupata haki zao za msingi.

Alisisitiza kuwa huduma hizi hazipaswi kucheleweshwa, na akaishauri Serikali kuongeza ufanisi katika taasisi hiyo, Ingawa majibu ya kina hayakuainishwa wazi, hoja yake ilibeba uzito wa kuamsha mjadala mpana juu ya uwajibikaji wa taasisi za umma.

Katika upande wa mafanikio, aliipongeza Serikali kwa kampeni ya Mama Samia Legal Aid Campaign, akibainisha mchango wake katika kusogeza huduma za kisheria kwa wananchi wa kawaida. Lakini kama ilivyo hulka ya uongozi makini, hakusimama kwenye pongezi alipendekeza kuanzishwa kwa mfuko maalum wa kusaidia gharama za usafiri na mahitaji ya msingi kwa wananchi wanaofuatilia kesi zao, pamoja na kuhimiza kasi ya usikilizwaji wa kesi mahakamani.

Nje ya ukumbi wa Bunge, Dkt. Majule aliendelea kuishi kile anachokiamini ushiriki wake katika matukio kama Bunge Marathon umeonesha kuwa uongozi hauishii kwenye hotuba, bali unahusisha uwepo wa karibu na jamii, kuhamasisha afya, mshikamano na umoja.

Kwa ujumla, Aprili 2026 si tu mwezi wa matukio, bali ni kioo kinachoonesha aina ya uongozi unaohitajika, uongozi unaounganisha sauti za wananchi na mifumo ya maamuzi, unaosukuma majibu kutoka kwa mamlaka, na unaoweka mbele maslahi ya watu.

Dkt. Neema Peter Majule anajitokeza kama kiongozi wa aina hiyo anayesikiliza kwa makini, anauliza kwa ujasiri, na anafuatilia kwa uthabiti hadi majibu yageuke kuwa matendo ni uongozi unaoleta matumaini unaojenga kesho iliyo bora.


Na Janeth Raphael- MichuziTv -Dodoma 

Tanzania imepata heshima kubwa ya kuwa mwenyeji wa Mkutano Mkuu wa Pili wa Mwaka wa Jumuiya za Wataalamu wa Usimamizi wa Rasilimaliwatu na Utawala Bora barani Afrika, tukio litakalowakutanisha wataalamu kutoka mataifa mbalimbali kwa lengo la kubadilishana uzoefu, kujengeana uwezo na kuimarisha mifumo ya utumishi wa umma katika bara la Afrika.

Mkutano huo mkubwa umepangwa kufanyika kuanzia tarehe 5 hadi 8 Mei, 2026 katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC), ambapo Tanzania itawakilishwa na taasisi zote zilizo chini ya Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Aprili 29, 2026 jijini Dodoma, Mwenyekiti wa African Association for Public Administration and Management (AAPAM) Tanzania Chapter, Leila Mavika, amesema maandalizi ya mkutano huo yamekamilika kwa kiwango kikubwa na unatarajiwa kuwa na matokeo chanya kwa maendeleo ya utawala bora barani Afrika.

Mavika alieleza kuwa mkutano huo umeandaliwa na AAPAM, taasisi inayojumuisha nchi zote wanachama barani Afrika kupitia matawi yake ya kitaifa, ambapo Tanzania ina AAPAM Tanzania Chapter inayoratibiwa chini ya Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma kama mlezi wa taasisi hiyo nchini.

Ameongeza kuwa mkutano huo wa pili wa mwaka utakuwa jukwaa muhimu la kitaaluma litakalowakutanisha wataalamu wa utawala wa umma, usimamizi wa rasilimaliwatu na utawala bora kutoka nchi mbalimbali za Afrika, kwa lengo la kujadili changamoto, fursa na mbinu bora za kuboresha utendaji wa sekta ya umma.

Aidha, Mavika amebainisha kuwa mkutano huo utashirikisha pia Jumuiya ya Wataalamu wa Utawala wa Umma na Usimamizi wa Rasilimaliwatu Tanzania (TAPAHR) pamoja na Mtandao wa Mameneja wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu Tanzania (TPS-HRMnet), katika kuimarisha ushirikiano wa kitaaluma na kikanda.

Katika hatua nyingine, ametoa wito kwa waajiri wote katika Wizara, Tawala za Mikoa, Mamlaka za Serikali za Mitaa, Wakala za Serikali, Mashirika ya Umma, Vyuo Vikuu na Vyuo vya Kati kuhakikisha wanawapatia wataalamu wao wa utumishi wa umma nafasi ya kushiriki kikamilifu katika mkutano huo.

Amesema ushiriki huo utawasaidia kuongeza ujuzi, kubadilishana uzoefu na kuimarisha utendaji kazi katika maeneo yao ya kazi, hatua ambayo itachangia kwa kiasi kikubwa kuboresha huduma kwa wananchi.

Mkutano huo unatarajiwa kuwa moja ya matukio makubwa ya kikanda katika mwaka 2026, ukiweka Tanzania katika ramani ya uongozi wa mijadala ya utawala bora na maendeleo ya rasilimaliwatu barani Afrika.




 

Waziri wa Elimu,Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda,akizungumza wakati akifungua  Mkutano wa 37 wa Baraza la Wafanyakazi wa wizara hiyo uliofanyika leo Aprili 29,2029 jijini Dodoma.

Waziri wa Elimu,Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda,akizungumza wakati akifungua  Mkutano wa 37 wa Baraza la Wafanyakazi wa wizara hiyo uliofanyika leo Aprili 29,2029 jijini Dodoma.

Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Nombo,akizungumza wakati wa   Mkutano wa 37 wa Baraza la Wafanyakazi wa wizara hiyo uliofanyika leo Aprili 29,2029 jijini Dodoma.

Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Nombo,akizungumza wakati wa   Mkutano wa 37 wa Baraza la Wafanyakazi wa wizara hiyo uliofanyika leo Aprili 29,2029 jijini Dodoma.

Sehemu ya washiriki wakimsikiliza Waziri wa Elimu,Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda (hayupo pichani) wakati wa  Mkutano wa 37 wa Baraza la Wafanyakazi wa wizara hiyo uliofanyika leo Aprili 29,2029 jijini Dodoma.

Waziri wa Elimu,Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda,akiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kufungua   Mkutano wa 37 wa Baraza la Wafanyakazi wa wizara hiyo uliofanyika leo Aprili 29,2029 jijini Dodoma.

Waziri wa Elimu,Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda,akiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kufungua   Mkutano wa 37 wa Baraza la Wafanyakazi wa wizara hiyo uliofanyika leo Aprili 29,2029 jijini Dodoma.

....

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda, amesema utekelezaji wa mageuzi ya elimu unaoendelea nchini ni sehemu ya dhamira thabiti ya Serikali ya Awamu ya Sita ya kuhakikisha vijana wanapatiwa ujuzi, maarifa na uwezo unaowawezesha kushiriki kikamilifu katika uchumi wa taifa.

Ameyasema hayo leo  Aprili 29, 2026 katika Mkutano wa 37 wa Baraza la Wafanyakazi wa wizara hiyo, Prof. Mkenda amesisitiza kuwa sekta ya elimu inabeba wajibu mkubwa katika maendeleo ya nchi na kwamba, wajibu wa Wizara ni kuhakikisha mipango yote inatekelezwa kwa ufanisi na kwa kasi.

Waziri Mkenda ameongeza kuwa kuanzishwa kwa Wizara maalum ya maendeleo ya vijana ni uthibitisho wa umuhimu wa kundi hilo katika maendeleo ya taifa na kuwa elimu ya ufundi kupitia VETA, ni msingi wa kuwaandaa vijana kuzalisha na kushiriki katika uchumi wa kisasa.  "Utekelezaji wa elimu ya miaka 10 ya lazima na uimarishaji wa shule za Sekondari na shule za amali unatekelezwa kwa ushirikiano wa karibu na Ofisi ya Rais – TAMISEMI, na hata sekta binafsi hasa katika kuhakikisha upatikanaji wa shule karibu na makazi ya wananchi na ununuzi wa vifaa vya kisasa kwa ajili ya mafunzo ya ufundi."amesema Prof. Mkenda Katika kuhimiza ubunifu na uwajibikaji, Prof. Mkenda amewataka watumishi wa Wizara kuendeleza kasi ya utendaji na kuhakikisha wananchi wanaendelea kupata taarifa kuhusu utekelezaji na mafanikio ya serikali katika maeneo ya sekta ya elimu, sayansi, teknolojia na ubunifu.

Kwa upande wake Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Nombo,amesema Serikali inaendelea kuimarisha usimamizi wa ajira na rasilimaliwatu kwa kuzingatia malengo na maono ya Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan hususan katika utekelezaji wa Kifungu cha 73 cha Sheria ya Ajira kinachohusu uhusiano kazini.

Prof. Nombo amesema kuwa kupitia mkutano huo, wajumbe watapitia mpango na bajeti ya wizara pamoja na masuala ya utawala na usimamizi wa rasilimali watu pamoja na kujadili masuala mbalimbali yanayolenga kuboresha afya na usalama mahali pa kazi. Prof. Nombo amesisitiza kuwa mshikamano na ushirikiano miongoni mwa wafanyakazi ni nguzo muhimu ya kufanikisha ubora na uaminifu katika utendaji kazi,  "Dhamira ya Wizara ni kuona watumishi wanafanya kazi kwa bidii, kwa uadilifu na kwa kuzingatia maadili ya utumishi wa umma ili kuendeleza mageuzi yanayoendelea katika elimu."amesema Prof. Nombo Aidha, amewashukuru wajumbe wa Baraza hilo kwa ushirikiano wao na amewataka kuendekeza juhudi za kuimarisha mifumo ya usimamizi ndani ya Wizara.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo na Waziri wa Mambo ya Nje wa Belarus, Maxim Ryzhenkov wakisaini mkataba wa makubaliano ya kushirikiana katika Uchumi, mkataba huo umesainiwa leo Aprili 29, 2026 jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo na Waziri wa Mambo ya Nje wa Belarus, Maxim Ryzhenkov wakionesha mkataba wa makubaliano ya kushirikiana katika Uchumi, mkataba huo ambao wameusaini leo Aprili 29, 2026 jijini Dar es Salaam.


SERIKALI ya Tanzania na Belarus zimesaini mkataba wa makubaliano (MoU) ya kuanzisha kamati maalumu ya ushirikiano wa kiuchumi na kibiashara, hatua inayolenga kuratibu mahusiano yao na kufungua ukurasa mpya wa maendeleo.

Makubaliano hayo yamesainiwa leo Aprili 29 2026 jijini Dar es Salaam na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo pamoja na Waziri wa Mambo ya Nje wa Belarus, Maxim Ryzhenkov.

Akizungumza baada ya kusaini ushirikiano huo, Profesa Kitila anasema hatua hiyo inalenga kufufua mahusiano kati ya Tanzania na Belarus ambayo yanasimama kwa takribani miaka 30 iliyopita.

Amesisitiza kuwa makubaliano hayo yanafungua fursa za uwekezaji kutoka Belarus katika sekta mbalimbali zikiwemo kilimo, viwanda na biashara, hali inayotarajiwa kuongeza ajira na mapato ya taifa.

Aidha, amesema ushirikiano huo utaisaidia Tanzania katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya 2050 kwa kuvutia wawekezaji wapya, kuleta teknolojia za kisasa na kuongeza ushindani wa uchumi.

Katika hatua nyingine, Profesa Mkumbo amebainisha kuwa kuna mpango wa kupeleka vijana nchini Belarus ili kujifunza teknolojia mbalimbali, hususani zitakazosaidia kuboresha sekta ya kilimo.

Kwa upande wake, Ryzhenkov amesema anafuraha sana kwamba wamesaini makubaliano ya kuanzisha Kamati ya Pamoja ya Biashara na Uchumi na hicho kitakuwa chombo muhimu kwa mahusiano yao.

Amesema wanaitazama Tanzania kama mshirika muhimu na lango lao kuu la ukuaji katika ukanda huu, hivyo wapo tayari kuwekeza katika miradi ambayo haitachochea tu biashara kati ya nchi zao, bali pia kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha kimkakati kwa biashara yetu barani Afrika.

“Tunaitazama Tanzania kama mshirika muhimu na lango letu kuu la ukuaji katika ukanda huu. Tuko tayari kuwekeza katika miradi itakayoiwezesha Tanzania kuwa kitovu cha kimkakati cha biashara barani Afrika,”amesema Ryzhenkov.

Amesema katika ziara yao, walitembelea maeneo kadhaa ya kuvutia, ikiwemo maeneo ya usindikaji wa bidhaa za mauzo ya nje na kwa sasa wanatafakari namna bora ya kushiriki kikamilifu katika mifumo hiyo.

Pia amesema kampuni kadhaa za Belarus zimeonyesha nia ya kutumia maeneo hayo hususani kuna nia ya kuanzisha kituo cha kikanda cha mbolea na bidhaa nyingine kitakachohudumia si Tanzania pekee bali pia ukanda mpana wa Afrika Mashariki.

Ryzhenkov amesema makubaliano mengine kadhaa ya msingi yako mezani kwa sasa lakini hadi kufikia ziara ya Waziri Mkuu wao Oktoba, mwaka huu watakuw awamekamilisha, makubaliano hayo yakiwemo ulizi wa uwekezaji na ushirikia no katika huduma za forodha.

Amesema mbali na biashara anatarajia kuona ushirikiano wao ukitanuka hadi kwenye masuala ya kibinadamu, mazungumzo ya kisiasa na mambo ya nje, yeye na wenzake na wamejizatiti kurahisisha mahusiano hayo na kuimarisha ushirikiano wa biashara kwa biashara pamoja na watu kwa watu

Pia amesema wako tayari kuanzisha mawasiliano ya moja kwa moja kati ya vyuo vikuu vya nchi zote na vituo vya utafiti ili kukuza miradi ya pamoja ya utafiti yenye manufaa kwa pande zote na kuleta karibu zaidi jumuiya za kisayansi za nchi zao.








Matukio mbalimbali.

Na Janeth Raphael- MichuziTv -Dodoma


Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda, amesema hana mpango wa kugombea cheo chochote cha uongozi na kwamba yuko tayari kuzungumza ukweli popote pale bila kuogopa, akisisitiza umuhimu wa uadilifu na uwajibikaji katika jamii.

Makonda ametoa kauli hiyo leo jijini Dodoma wakati wa uzinduzi wa Mkakati wa Taifa wa Kukabiliana na Mmomonyoko wa Maadili, mkakati unaolenga kurejesha na kuimarisha misingi ya maadili katika jamii ya Watanzania, hususan kwa vijana.

Akizungumza mbele ya wadau mbalimbali, Makonda amewataka wanahabari kubadili namna ya uandishi wa habari, akisema kwa sasa baadhi ya vyombo vya habari vimejikita zaidi katika kuripoti matukio yenye mwelekeo wa kushtua na kuvutia hisia, badala ya kuangazia habari zenye kujenga taifa.

Amesema matukio kama vifo, ufumaniaji na migogoro ya kijamii yamekuwa yakipewa nafasi kubwa zaidi kwenye mitandao na vyombo vya habari, hali ambayo kwa mujibu wake inaweza kuchangia mmomonyoko wa maadili kwa jamii.

“Kwa nini hamuelezi mazuri yanayofanywa na nchi hii? Chagueni habari zenye maadili ya Watanzania,” amesema Makonda, akisisitiza kuwa uandishi wa habari unapaswa kuwa na uwiano unaojenga na si kubomoa jamii.

Aidha, ameeleza kuwa hata baadhi ya viongozi wa dini wameanza kujihusisha zaidi na kutafuta matukio yanayovutia mitandaoni badala ya kuzingatia jukumu lao la msingi la kuhubiri maadili na kuelimisha jamii, hasa watoto na vijana.

Amesema ni muhimu kwa viongozi hao kurejea kwenye msingi wa malezi ya kiroho na kijamii kwa kujikita zaidi katika shughuli za mafunzo ya maadili mashuleni, kwenye taasisi za dini na katika jamii kwa ujumla.

Makonda pia amesisitiza kuwa vyombo vya habari vina nguvu kubwa ya kuathiri fikra na mienendo ya jamii, hivyo vinapaswa kuitumia nafasi hiyo kwa busara ili kuhamasisha maadili mema, uzalendo na mshikamano wa kitaifa.

Ameongeza kuwa mkakati huo wa taifa utahusisha wadau mbalimbali wakiwemo serikali, taasisi za dini, vyombo vya habari na jamii kwa ujumla katika kuhakikisha maadili yanarejea na kudumishwa.

Uzinduzi wa mkakati huo umeelezwa kuwa ni hatua muhimu katika kukabiliana na changamoto za kijamii zinazoongezeka, zikiwemo mmomonyoko wa maadili miongoni mwa vijana, matumizi mabaya ya mitandao ya kijamii na kupungua kwa malezi ya kijamii.








Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma


Serikali imeendelea kusisitiza dhamira yake ya kuhakikisha shule zote za msingi na sekondari nchini zinakuwa jumuishi, ili kutoa fursa sawa za elimu kwa wanafunzi wote wakiwemo wenye mahitaji maalum.

Hayo yameelezwa na Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Dkt. Festo Ndugange, alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Aisha Msantu Mduyah, aliyekuwa akitaka kufahamu mikakati ya serikali katika kuboresha miundombinu wezeshi kwa wanafunzi wenye mahitaji maalum.

Dkt. Ndugange amesema kuwa hatua hiyo inatekelezwa kwa mujibu wa Mwongozo wa Utekelezaji wa Mkakati wa Elimu Jumuishi wa mwaka 2022–2026 pamoja na Waraka Namba 3 wa mwaka 2025, unaolenga kuimarisha mfumo wa kitaifa wa kuzifanya shule kuwa jumuishi.

Ameeleza kuwa serikali imeweka mikakati mbalimbali kuhakikisha wanafunzi wenye mahitaji maalum wanapata mazingira bora ya kujifunzia na kuendeleza vipaji vyao. Mikakati hiyo ni pamoja na ujenzi wa miundombinu rafiki kwa wanafunzi hao, ikiwemo madarasa, vyoo na njia za kupita zinazokidhi mahitaji yao.

Aidha, serikali inaendelea kuhakikisha bajeti zake zinatenga fedha kwa ajili ya ununuzi wa vifaa wezeshi na visaidizi, vinavyosaidia ujifunzaji kwa wanafunzi wenye changamoto mbalimbali. Vifaa hivyo vinajumuisha zana za kufundishia na kujifunzia zinazowezesha ushiriki kamili darasani.

Katika kuimarisha rasilimali watu, serikali pia inaendelea kuajiri walimu wenye utaalamu wa elimu maalum pamoja na kutoa mafunzo kwa walimu waliopo ili kuwajengea uwezo wa kushughulikia wanafunzi wenye mahitaji maalum kwa ufanisi zaidi.

Akitoa takwimu za hali ya sasa, Dkt. Ndugange amesema kuwa kuna shule maalum 44 za msingi na shule moja ya sekondari, sambamba na vitengo maalum 815 katika shule za awali na msingi. Pia kuna jumla ya shule jumuishi 20,889 za msingi na 6,488 za sekondari kote nchini.

Kwa upande wa wanafunzi wenye changamoto kubwa zaidi, serikali imeanzisha shule jumuishi za sekondari za bweni 53 za kitaifa pamoja na shule 3 za kutwa, ambazo zinapokea wanafunzi hao kutoka maeneo mbalimbali ya nchi.

Ameongeza kuwa serikali itaendelea kuboresha miundombinu na huduma katika shule zote ili kuhakikisha zinakuwa jumuishi zaidi, na kwamba hakuna mwanafunzi atakayebaki nyuma katika kupata elimu bora kutokana na changamoto alizonazo.

Hatua hizi zinaonyesha dhamira ya serikali ya kujenga mfumo wa elimu unaozingatia usawa, ujumuishi na fursa kwa wote, huku ikiwapa wanafunzi wenye mahitaji maalum nafasi ya kufikia ndoto zao kulingana na uwezo na vipaji vyao.


 


Taasisi ya Saratani Ocean Road imeendelea kutoa elimu na huduma za uchunguzi wa saratani mbali mbali katika Maadhimisho ya Wiki ya Afya Kitaifa 2026.

Kilele cha maadhimisho hayo yamefanyika katika viwanja vya Shule ya Sekondari Zimbwini, Kibiti Mkoa wa Pwani, ambapo mgeni rasmi ni Waziri wa Afya, Mohamed Mchengerwa, ambayo ni maaluku kwa chanjo, Bima Afya kwa wote na usafi wa mazingira.

Akizungumza katika maadhimisho hayo, Meneja wa Huduma za Uchunguzi wa Saratani na Elimu kwa Umma, DK. Maguha Stephano, amesema taasisi hiyo inaunga mkono juhudi za serikali kuhakikisha  wananchi wanapata elimu kuhusu saratani.

Maguha amesema pia wanahakikisha wananchi wanapata chanjo zinazozuia maambukizi ya virus I vinavyosababisha saratani za mlango wa kizazi, saratani ya  ini na huduma za uchunguzi wa saratani mbali mbali, zikiwemo mlango wa kizazi, matiti na tezi Dume kwa wanaume.

Amesema Saratani ya tezi Dume inafanyika kwa njia ya kipimo cha damu na huduma hizo zinatolewa bila malipo na taasisi hiyo.

Aidha Maguha amewaomba wananchi wa Mkoa wa Pwani katika katika Wilaya ya Kibiti kutumia fursa hiyo  kupata huduma hizo bure.




 Na Leandra Gabriel, Michuzi TV

KATIKA Kuendelea kuboresha huduma kwa watanzania Shirika La Mawasiliano Tanzania (TTCL,) kupitia faida ya Shilingi Bilioni 22.98 iliyotengeneza kwa mwaka wa fedha 2024/2025 limenunua na kukabidhi idara ya ufundi magari tisa aina ya Hilux yenye thamani ya Shilingi Bilioni 1.6 pamoja na bajaji 28 zenye thamani ya shilingi  milioni 291.2 na kuzielekeza idara na vitengo kutumia vitendea kazi hivyo kwa kuwafikia na kutoa huduma kwa wakati kwa wateja na kufikia malengo ya kuwaunganisha na huduma wateja milioni moja kwa kipindi cha miaka mitatu.

Akizungumza leo jijini Dar es Salaam wakati wa kukabidhi magari na bajaji hizo kwa wakuu wa Idara na Vitengo vya Shirika hilo Mkurugenzi mkuu wa TTCL Moremi Marwa amesema, vitendea kazi hivyo vimelenga kuwafikia kwa wakati wateja wanaotumia huduma kutoka Shirika hilo ikiwemo watumiaji wa huduma ya Faiba Mlangoni kwako.

`` Magari pamoja na bajaji hizi zitatumiwa na mafundi na watumishi wanaohudumia wateja, pindi huduma zinapokatika au wateja kupata hitilafu katika utumiaji wa huduma mafundi wetu watawafikia kwa wakati na kutatua changamoto na kwa ufanisi zaidi. “Amefafanua.”

Aidha amesema; Shirika hilo pia limenunua magari matano aina ya Hiace ambayo yatapokelewa mwisho wa mwezi huu mahususi kwa ajili ya masoko na mauzo kwa kuwafikia wateja wao pamoja na kuwafikia wateja wapya na kufafanua kuwa vifaa hivyo ni sehemu ya faida iliyotengenezwa na Shirika hilo ili kuweza kuhudumia wateja wao kwa ufanisi zaidi na kupata mapato yatakayoendeleza Shirika na kutoa gawio kwa Serikali.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa ufundi wa TTCL Mhandisi. Cecil Francis amemshukuru Mkurugenzi mkuu wa Shirika hilo kwa kusimamia maamuzi hayo ya kimkakati kwa kuhakikisha kunakuwa na vitendea kazi vitakavyorahisisha utoaji huduma na kuwafikia wateja wengi zaidi na kuwataka wafanyakazi wa Shirika hususani Idara ya ufundi kuvitumia vitendea kazi hivyo kwa madhumuni yaliyowekwa ili kuleta tija kwa Shirika na watumiaji wa huduma za TTCL.

Cecil ameeleza kuwa wamejidhatiti katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora na kwa wakati pamoja na kuhakikisha wanafikia mikoa yote nchini na kuhakikisha azma ya Serikali ya kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya mawasiliano na kuendana na kasi ya ukuaji wa teknolojia inatimia.

Mkurugenzi wa Shirika La Mawasiliano Tanzania (TTCL,) Moremi Marwa akizungumza wakati akikabidhi magari na bajaji hizo kwa Idara na Vitengo na kuwasisitiza kutumia vitendea kazi hivyo kwa malengo na kuleta matokeo chanya katika utoaji huduma. Leo jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi wa Shirika La Mawasiliano Tanzania (TTCL,) Moremi Marwa (kulia,) akikabidhi mfano wa funguo kwa Mkurugenzi wa Biashara wa Shirika hilo Vedastus Mwita (kushoto,) Leo jijini Dar es Salaam.


Mkurugenzi wa Shirika La Mawasiliano Tanzania (TTCL,) Moremi Marwa (kulia,) akikabidhi mfano wa funguo kwa Mkurugenzi wa Ufundi wa Shirika hilo Mhandisi. Cecil Francis (kushoto,) Leo jijini Dar es Salaam.

SERIKALI imesema uzalishaji na uingizaji wa mifuko ya plastiki iliyopigwa marufuku umepungua kwa asilimia 95 hatua iliyochangia kupungua kwa uzalishaji wa taka za plastiki katika maeneo mbalimbali nchini.

Hayo yamesemwa na Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Reuben Kwagilwa bungeni jijini Dodoma leo Aprili 29, 2026, wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalumu Mhe. Dkt. Catherine Joachim aliyetaka kujua Serikali imepata matokeo gani katika kupunguza uchafuzi wa mazingira tangu kuanza kwa katazo la matumizi ya mifuko ya plastiki mwaka 2019.

Akijibu swali hilo Mhe. Kwagilwa alibainisha kuwa baada ya katazo hilo kiwango cha uelewa wa wananchi kuhusu madhara ya plastiki kiliongezeka kutoka kutoka chini ya asilimia 40 mwaka 2018 hadi kufikia zaidi ya asilimia 85 mwaka 2026.

Kutokana na hatua hiyo, alitoa rai kwa wananchi kuendelea kuzingatia katazo la matumizi ya mifuko ya plastiki kwa ajili ya kulinda afya na kuhifadhi mazingira kwa maendeleo endelevu ya kizazi cha sasa na kijacho.

Aidha, Naibu Waziri huyo aliongeza kuwa taka za plastiki katika maeneo ya fukwe za bahari na maziwa zimepungua kwa takribani asilimia 60 hivyo kupunguza hatari kwa viumbe wa majini.

Halikadhalika, Mhe. Kwagilwa alieleza kuwa katazo la mifuko ya plastiki limesaidia kupungua kwa gharama za kuzibua mitaro ya maji machafu kwa wastani wa asilimia 30 hadi 40, kwani mifuko ya plastiki ilikuwa chanzo kikuu cha uzibaji wa miundombinu hiyo.

Akijibu maswali ya nyongeza, alibainisha kuwa Serikali imeweka jitihada madhubuti za kuhakikisha taka hususani zile za plastiki zinazozalishwa katika maeneo mbalimbali nchini zinarejelezwa na kuzalisha bidhaa.

Pia, alisema Serikali inahakikisha kwenye majiji kwa mfano Dar es Salaam, inajenga madampo makubwa yatakayoambatana na viwanda vitakavyofanya shughuli ya urejelezaji na kuchakata taka kuwa bidhaa, hatua itakayosaidia kudhibiti taka.

Ifahamike kuwa mifuko ya plastiki ni aina ya mifuko yenye mchanganyiko wa kemikali zisizooza hivyo kuleta athari kwenye mazingira pamoja na afya kwa binadamu na wanyama.

Aidha, kutokana na tafiti mbalimbali mifuko ya plastiki huchukua miaka 400 hadi 1000 kuoza ardhini na hivyo kuleta athari mbalimbali zikiwemo kuathiri mifumo ikolojia ya bahari ambapo inakadiriwa 100,000 viumbe bahari na ndege bahari millioni moja kila mwaka wanakufa kwa kula mifuko ya plastiki.

Athari zingine ni pamoja na kuchafua miji kutokana na kushindwa kuoza, kuathiri mifugo kutokana na kula mifuko ya plastiki, kuharibu miundombinu kwa kuziba kwenye mifereji na baadhi ya njia za maji, kubeba na kusambaza viumbe vamizi na bakteria na pia inapochomwa moshi wake una madhara na unaweza kusababisha maradhi ya kansa.



MAAFISA Usafirishaji maarufu kwa jina la Bodaboda wa Wilaya ya Kyela Mkoa wa Mbeya wahimizwa kushirikiana na Jeshi la Polisi kubaini, kuzuia na kutanzua uhalifu katika maeneo yao.

Wito huo umetolewa na Mkuu wa Wilaya ya Kyela Mhe Josephine Manase Aprili 28, 2026 wakati akifungua mashindano ya Mpira wa Miguu ya "Kyela Polisi Jamii Bodaboda Super Cup, 2026 yaliyokuwa yakifanyika katika uwanja wa Polisi Kyela na kushirikisha Maafisa Usafirishaji wa Wilaya hiyo kutoka katika Kata 33.

Mhe Manase amewataka wananchi wa Wilaya hiyo kuilinda Amani iliyopo kwa kuacha na kujiepusha kujihusisha na makundi yasiyofaa, vitendo visivyofaa katika jamii na badala yake washirikiane na Jeshi la Polisi kuimarisha ulinzi na usalama pamoja na kufichua wahalifu.

Aidha, Mhe Manase amepongeza mikakati thabiti ya Jeshi la Polisi Wilayani humo katika kuzuia uhalifu kupitia utekelezaji wa falsafa ya Polisi Jamii ambayo imekuwa ikishirikisha wananchi, kuwajengea uwezo na uelewa wa masuala ya usalama hali inayopelekea kupata mafanikio katika kuzuia uhalifu.

Mkuu wa kitengo cha ushirikishwaji wa Jamii, Naibu Kamishna wa Polisi (DCP) Henry Mwaibambe kutoka Makao Makuu ya Polisi Dodoma amewasihi wananchi wa Kyela kuilinda Amani iliyopo na kuacha kusikiliza maneno yenye nia ya kuvuruga amani na utulivu uliopo kwani kwenye amani watakuwa huru kufanya kazi zao za uzalishaji mali.

Naye, Diwani wa Kata ya Mikoroshini Gwakisa Mwakipesile amesema kuwa mashindano hayo yamekuwa na faida kubwa kwa vijana hasa Bodaboda kwani yamerejesha imani kati ya Jeshi la Polisi na Wananchi wa Kyela ambapo ushirikiano huo ni ishara ya mahusiano mazuri katika kukabiliana na uhalifu.

Kwa upande wake, Joshua Mwaisumo, Mkazi wa Kyela amepongeza waandaaji wa mashindano hayo kwani yamesaidia kuisogeza jamii karibu na Jeshi la Polisi na kusaidia jamii kupata elimu, kutoa taarifa za uhalifu na wahalifu na hatimaye Kyela kuwa salama.

Fainali ya mashindano hayo yalizikutanisha timu za Bodaboda Kata ya Ipinda dhidi ya Bodaboda Kata ya Serengeti na kushuhudia Bodaboda Kata ya Ipinda kuibuka mabingwa kwa changamoto za penati 5 kwa 3 na kuzawadi Ng'ombe, Jezi na Mpira. Mashindano hayo yalibeba ujumbe unaosema, "Amani, Utulivu na Mshikamano, kwa usalama na Maendeleo yetu"
 




WAZIRI wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda amezindua makati wa Taifa wa Kukabiliana na Mmomonyoko wa Maadili wa mwaka 2026/27 hadi 2036/37, akisema hatua hiyo ni muhimu katika kulinda mustakabali wa Taifa.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Makonda amesema mkakati huo unatekeleza maelekezo ya Rais Samia Suluhu Hassan aliyoyatoa Septemba 24, 2024 mkoani Ruvuma wakati wa Tamasha la Tatu la Kitaifa la Utamaduni, ambapo alielekeza kuandaliwa mfumo wa pamoja wa kitaifa utakaounganisha nguvu za Serikali, familia na wadau wote kulinda utambulisho wa Watanzania.

Amesema maadili ni msingi mkuu wa maendeleo ya nchi yoyote, yakitoa mwelekeo wa fikra, mienendo na maamuzi ya jamii katika nyanja zote, huku akibainisha kuwa Katiba ya mwaka 1977 kupitia Ibara ya 9 inaweka misingi ya Utu, Umoja, Usawa, Utaifa na Uwajibikaji kama nguzo za maisha ya Mtanzania.

Makonda amesema licha ya fursa zinazotokana na maendeleo ya sayansi, teknolojia na utandawazi, bado kuna changamoto ya mmomonyoko wa maadili ikiwemo kupungua kwa uwajibikaji, kudhoofika kwa taasisi ya familia, matumizi yasiyofaa ya mitandao, kuongezeka kwa uhalifu, matumizi ya dawa za kulevya na vitendo vya ukatili dhidi ya watoto na makundi mbalimbali.

Kutokana na hali hiyo, Serikali imeandaa mkakati wa miaka 10 unaolenga kujenga jamii yenye maadili imara inayozingatia utu, uwajibikaji, uzalendo na mshikamano wa kitaifa". Amesema Makonda

Amesema kuwa mkakati huo umezingatia maeneo muhimu ikiwemo kuimarisha taasisi ya familia, kuboresha urithishaji wa maadili kupitia elimu, kuhamasisha matumizi sahihi ya teknolojia na mitandao, pamoja na kuimarisha usimamizi wa sheria na kanuni zinazolinda maadili ya jamii.

Amesema mkakati huo umeandaliwa kwa ushirikishwaji wa wadau mbalimbali kutoka Serikalini, sekta binafsi, taasisi za dini, wasanii, vijana na jamii kwa ujumla ili kuhakikisha unakuwa na uhalisia na umiliki wa pamoja.

Aidha, Makonda ametoa wito kwa Watanzania kushiriki kikamilifu katika kulinda na kuendeleza maadili, akisisitiza kuwa zaidi ya asilimia 42 ya Watanzania ni watoto na vijana wenye umri chini ya miaka 15, hivyo kuna wajibu wa pamoja kujenga msingi imara wa kimaadili kwa kundi hilo.

Amewataka wazazi na walezi kuwajibika katika malezi, viongozi wa dini na jamii kuhamasisha maadili, wasanii na wazalishaji wa maudhui kuzalisha kazi zinazojenga jamii, vyombo vya habari kuelimisha umma, na mamlaka za udhibiti kuimarisha utekelezaji wa sheria.

"Utekelezaji wa mkakati huu utaanzia ngazi ya familia hadi Taifa, Serikali inaahidi kuhakikisha wadau wote wanapata elimu na taarifa za mkakati huo kupitia majukwaa mbalimbali ikiwemo mitandao ya kijamii kwani bila maadili imara, maendeleo endelevu hayawezi kufikiwa.

Top News