Mgeni rasmi
-Yazingumzia pia uwekezaji mkubwa uliofanywa na Serikali katika hospitali hiyo,idadi ya wagonjwa waliohudumiwa
Na Said Mwishehe,Michuzi TV
UONGOZI wa Hospitali ya Benjamin Mkapa umeanza rasmi maandalizi ya maadhimisho ya miaka 10 tangu kuanzishwa kwake, sambamba na uzinduzi wa harambee ya kuchangisha fedha kwa ajili ya kuwa na Mfuko maalum utakaowezesha huduma za matibabu ya upandikizaji uloto kwa watoto wenye ugonjwa wa selimundu pamoja na huduma za upandikizaji figo.
Akizungumza leo katika kikao na Wahariri wa vyombo mbalimbali vya habari jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Benjamin Mkapa, Profesa Abel Makubi, amesema hospitali hiyo imeendelea kuwa tegemeo kubwa kwa wananchi kwa kuhudumia takribani watu milioni 10 kutoka mikoa mbalimbali ya Tanzania pamoja na wagonjwa kutoka nje ya nchi.
Amesema kwamba Julai 15, 2026, katika kilele cha maadhimisho ya miaka 10 ya hospitali hiyo, wanatarajia kufanya harambee yenye lengo la kupanua huduma za kibingwa, ambapo mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Kutokana na hali hiyo, Prof. Makubi amesema pia hospitali hiyo imekuwa moja ya vituo muhimu vya tiba utalii nchini huku akifafanua kupitia harambee hiyo, hospitali inalenga kukusanya jumla ya Shilingi bilioni 7 ndani ya kipindi cha miaka miwili, fedha zitakazosaidia kugharamia matibabu kwa wagonjwa 100.
“Kati yao, watoto 50 wanatarajiwa kufaidika na matibabu ya selimundu kupitia upandikizaji uloto, huku wagonjwa wengine 50 wakipatiwa huduma ya upandikizaji figo,” amesema Prof. Makubi na kuongeza tayari Sh.bilioni zimeshapatikana hivyo wanaendelea kuziomba taasisi za umma na binafsi pamoja na wananchi kuchangia kwa hiyari katika mfuko huo.
Hata hivyo, Prof. Makubi aliishukuru Ofisi ya Msajili wa Hazina pamoja na taasisi zake ambazo, kwa kushirikiana na wadau wengine, zimefanikiwa kuchangia kiasi cha Shilingi bilioni 4 hadi sasa.
“Kama mnavyofahamu, gharama za matibabu ni kubwa sana kwa wagonjwa. Tuna kila sababu ya kuendelea kumshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye alichangia Shilingi bilioni moja nje ya bajeti kwa ajili ya matibabu ya wagonjwa mbalimbali.
“Mchango huo ulisaidia wagonjwa waliokuwa hawana uwezo wa kugharamia matibabu yao, ambapo yeye alilipia gharama zote. Jambo hilo lilirejesha furaha kwa watoto, familia zao pamoja na wagonjwa wa figo waliopatiwa matibabu.”
Kuhusu mafanikio ya hospitali hiyo amesema kwa sasa ina watumishi 1,073, wakiwamo madaktari bingwa 100 sambamba na kuwa na vitanda 450 kwa ajili ya huduma za wagonjwa.
Pia amesema kwa sasa inatoa huduma za kibingwa 20, zikiwamo huduma za kibingwa za juu 18. Baadhi ya huduma hizo ni upandikizaji uloto, upasuaji wa moyo kwa kufungua kifua, uchunguzi wa moyo, kuzibua mishipa ya damu, upasuaji wa uti wa mgongo, upasuaji kwa kutumia matundu madogo pamoja na ubadilishaji wa nyonga na magoti.
“Hospitali imepata mafanikio makubwa kutokana na uwekezaji wa Serikali kuanzia awamu ya nne hadi ya sita, ambapo kiasi cha Shilingi bilioni 283 kimewekezwa katika majengo na vifaa tiba.
“Hivyo, unaweza kuona namna hospitali ilivyojidhatiti katika kuimarisha na kuboresha huduma za afya,” amesema huku akisisitiza hospitali hiyo imeendelea kutoa huduma za tiba utalii kwa raia kutoka nje ya nchi, ambapo baadhi yao huja moja kwa moja kufuata huduma hospitalini hapo.
“Kwa mfano, mwaka jana tuliwahudumia wagonjwa 2,897 kutoka Burundi. Pia wapo wagonjwa wanaokuja moja kwa moja kutoka nchini humo pamoja na wengine kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.”
Ametaja mafanikio mengine ni kufanyika kwa maboresho makubwa ya mifumo ya TEHAMA ambayo imerahisisha utoaji wa huduma bora kuanzia usajili wa wagonjwa. Pia wameanza makundi matano ya huduma huru yanayowezesha mawasiliano ya moja kwa moja na wagonjwa.


.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)



.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)










.jpeg)

.jpeg)






.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)



.jpeg)





.jpeg)





