Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amesema mradi wa ujenzi wa Maabara za Sayansi na Skuli ya Kilimo ya Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) ni muhimu kwa kuwa unaolenga kuweka misingi imara ya maendeleo ya Teknolojia, Ujuzi, na Uchumi katika jamii.

 Makamu wa Rais amesema hayo wakati akiweka Jiwe la Msingi la ujenzi wa Maabara za Sayansi na Skuli ya Kilimo ya Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) ikiwa ni shamrashamra za Miaka 62 ya Muungano.

 Amesema mradi huo utaleta manufaa makubwa kwa nchi, ikiwa ni pamoja na kutengeneza fursa za ajira, kuongeza uelewa katika sayansi na teknolojia, kushajihisha uchumi wa buluu na kuongeza tija katika kilimo.

 Aidha, Makamu wa Rais amesema elimu ni kipaumbele cha Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuwa ndiyo inayowezesha uendelezaji wa rasilimaliwatu ili kuchangia kikamilifu katika kujenga Taifa na kuleta maendeleo kwa ujumla. 

Ameongeza kwamba uwekaji wa Jiwe la Msingi unaangazia mafanikio ya Muungano wa Tanzania katika miaka 62 iliyopita, ambapo umewezesha kushirikiana zaidi, kuimarisha amani, na kustawisha maendeleo ya kiuchumi na kijamii katika pande zote mbili za Muungano.

 Makamu wa Rais ametoa wito kwa Mshauri Elekezi na Mkandarasi wa mradi huo, kusimamia kikamilifu utekelezaji wa mradi na kuhakikisha unafikia malengo yaliyokusudiwa. Amesema ni matarajio kuona mradi unatekelezwa kwa kuzingatia viwango vya hali ya juu, weledi, thamani ya fedha na kukamilika kwa wakati.

Vilevile ametoa rai kwa uongozi wa SUZA kusimamia rasilimali hizo kwa uadilifu na uwazi ili kuhakikisha kuwa miundombinu inayojengwa inawezesha kufikiwa kwa malengo yaliyokusudiwa, ikiwemo kuchochea tafiti na bunifu zinazolenga kutatua changamoto halisi za jamii, hususan katika sekta za kilimo, teknolojia, utalii na mazingira. 

Kwa upande wake Kaimu Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) Prof. Abdi Talib Abdalla amesema Jengo la Maabara ya Sayansi litakuwa kitovu muhimu katika ufundishaji wa sayansi tafiti za kisasa, bunifu na teknolojia ndani ya chuo na nchi kwa ujumla

 Amesema kupitia maabara hizo za kisasa wanafunzi na watafiti watapata mazingira bora ya kufanya majaribio tafiti shirikishi na bunifu zinazolenga kutatua changamoto mbalimbali za kijamii kiuchumi na kimazingira. 

Aidha uwekezaji huo utaongeza ubora wa elimu ya sayansi na kuzalisha wataalamu wenye ujuzi wa vitendo na uwezo wa kushindana katika soko la ajira la kitaifa na kimataifa.

 Pia amesema Maabara na Skuli ya Kilimo itaimarisha uwezo wa Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar katika kutoa huduma za ushauri elekezi, mafunzo maalum na tafiiti zinazolenga kutatua changamoto za jamii na kuchochea uchumi wa Taifa.

Mradi Maabara na Skuli ya Kilimo wa Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar umefadhiliwa na mradi wa Benki ya Dunia wa HEET (The Higher Education for Economic Transformation - HEET), ambapo unagharimu kiasi cha shilingi bilioni 32.155.





 

Na. Josephine Majura, WF, Dodoma

Serikali kupitia Mamlaka ya Mapato (TRA), itaendelea kutathmini na kufuatilia kwa karibu ukuaji wa mapato ya kodi, ongezeko la idadi ya walipakodi na shughuli za kiuchumi katika Wilaya ya Karatu, mkoani Arusha, ili pale vigezo vitakapokamilika hatua stahiki ziweze kuchukuliwa ikiwemo kuipandisha hadhi kuwa mkoa wa kikodi.

Hayo yameelezwa bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Fedha Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum Mhe. Cecilia Paresso, aliyetaka kujua lini Serikali itaanzisha Mkoa wa Kikodi katika Wilaya ya Karatu.

Mhandisi Munde, alifafanua kuwa uanzishwaji wa mikoa ya kikodi hufanyika kwa kuzingatia vigezo vya kiutawala na kiuchumi ikiwemo kiasi cha mapato kinachokusanywa, idadi ya walipakodi, rasilimali zilizopo na mahitaji ya huduma katika eneo husika ili kuboresha utoaji wa huduma na kuongeza ufanisi wa ukusanyaji wa mapato ya kodi.

Aidha, alisema kuwa katika kuongeza ufanisi na kusogeza huduma kwa walipakodi, Serikali kupitia Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ilizipandisha hadhi baadhi ya wilaya za kikodi kuwa mikoa ya kikodi, ikiwemo Mkoa wa Kikodi wa Ilala, Kinondoni, Temeke, Kariakoo, Kahama, Tegeta na Pemba.

Mhandisi Munde, aliongeza kuwa Wilaya hizo zilizopewa hadhi ya mikoa ya kikodi zina wastani wa jumla ya walipakodi 906,399 (Ilala), 734,984 (Kinondoni), 563,568 (Temeke), 67,996 (Kariakoo), 82,054 (Kahama), 136,164 (Tegeta), na 28,076 (Pemba).

Kadhalika, katika mwaka wa fedha 2023/24 na 2024/25 wilaya hizo zilikuwa na wastani wa mapato ya kodi ya sh. bilioni 862.42 (Ilala), 574.36 (Kinondoni), 190.32 (Temeke), 136.03 (Kariakoo), 25.89 (Kahama), 101.1 (Tegeta), na 16.36 (Pemba).

“Kwa muundo wa kikodi wa sasa, Wilaya ya Karatu inatambulika kama wilaya ya kikodi chini ya mkoa wa kikodi wa Arusha ndani ya Idara ya Kodi za Ndani ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA)”, alisema Mhandisi Munde.

Wilaya ya Karatu ina jumla ya walipa kodi 4,672 ambao kwa kiasi kikubwa wanachangia ukusanyaji wa mapato ya kodi kutoka katika shughuli za utalii, madini na kilimo. Kadhalika, takwimu zinabainisha ukuaji wa asilimia 9.48 wa mapato ya kodi katika Wilaya hiyo, kwa kuzingatia makusanyo yenye jumla ya shilingi bilioni 10.07 kwa mwaka 2023/24 na sh. bilioni 11.12 kwa mwaka 2024/25.

Naibu Waziri wa Fedha Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum Mhe. Cecilia Paresso, aliyetaka kujua lini Serikali itaanzisha Mkoa wa Kikodi katika Wilaya ya Karatu, mkoani Arusha.

Serikali imewataka Wakaguzi Wakuu wa Migodi pamoja na Mameneja wa Migodi nchini kuwa mabalozi wa utekelezaji wa sheria, kanuni za madini na kuwa wazalendo katika biashara ya madini ili kuongeza mchango wa sekta hiyo kwenye uchumi wa taifa.

Wito huo umetolewa leo Aprili 24, 2026 wilayani Kahama, mkoani Shinyanga na Mtaalam kutoka Kurugenzi ya Ukaguzi na Biashara ya Madini  Tume ya Madini, Mhandisi Erasmina Massawe, kwenye mafunzo kwa Mameneja na Wakaguzi Wakuu wa Migodi ya uchimbaji mdogo yaliyowakutanisha washiriki kutoka mikoa ya kimadini ya Kahama, Mbogwe na Shinyanga.

Mafunzo hayo yamelenga kuimarisha uelewa wa kitaalam, usimamizi bora wa migodi, uzingatiaji wa sheria na kanuni za madini pamoja na kukuza uchimbaji salama na endelevu.

Amesema mbali na kujifunza mbinu za kuimarisha usalama migodini, viongozi hao wanapaswa kuwa sehemu ya mikakati ya Serikali ya kuhakikisha biashara ya madini inafanyika kwa uwazi na kwa kuzingatia Sheria ya Madini na kanuni zake, hatua itakayosaidia kudhibiti vitendo vya utoroshaji wa madini.

Ameeleza kuwa Serikali kupitia Tume ya Madini imeendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ya kuimarisha usimamizi wa biashara ya madini, ikiwemo uboreshaji wa mfumo wa biashara ya madini, uanzishwaji wa masoko na vituo vya ununuzi wa madini, uwepo wa Maafisa Migodi Wakazi katika maeneo ya uchimbaji pamoja na ujenzi wa ukuta wa Mirerani uliosaidia kudhibiti utoroshaji wa madini ya Tanzanite.

Aidha, amesema Serikali imeimarisha ulinzi na ufuatiliaji wa madini kwa kuweka wakaguzi katika maeneo muhimu kama viwanja vya ndege, bandari, mipakani na katika maeneo yote ya uzalishaji madini, sambamba na kusimamia utoaji wa vibali vya usafirishaji wa madini na utekelezaji wa Sheria ya kodi ikiwemo ondoleo la Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) kwenye baadhi ya shughuli za madini.

Akizungumzia uwezeshaji wa Watanzania kushiriki kikamilifu katika sekta hiyo, Mhandisi Massawe amesema maboresho ya Kanuni za Ushirikishwaji wa Watanzania katika Sekta ya Madini yameongeza kwa kiasi kikubwa ushiriki wa watanzania katika usambazaji wa bidhaa na  utoaji wa huduma mbalimbali migodini.

“Kwa sasa zipo fursa nyingi katika Sekta ya Madini ikiwemo huduma za chakula, ulinzi, vifaa kinga, huduma za kisheria, ujenzi na bima. Watanzania wanapaswa kuzitumia fursa hizi kujiongezea kipato na kukuza uchumi wa nchi,” amesisitiza.

Wakati huohuo amehimiza wadau wa madini nchini kutumia maabara bora ya Tume ya Madini iliyopo jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kupimiwa madini yao na sampluli za madini ili kufanya biashara ya madini ya uhakika.

Mafunzo hayo ni sehemu ya juhudi za Serikali kuimarisha usimamizi wa uchimbaji mdogo na kuhakikisha rasilimali za madini zinaleta manufaa mapana kwa wananchi na Taifa kwa ujumla.






Na MWANDISHI WETU

MWENGE wa Uhuru umeridhia miradi saba ya maendeleo yenye thamani ya zaidi ya sh. bilioni 13.3 iliyotekelezwa wilayani Kisarawe, mkoani Pwani na kumpongeza Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, kwa utekelezaji wa miradi hiyo.

Akizungumza katika mbio za Mwenge wa Uhuru wilayani humo, Kiongozi wa Mbio za Mwenge Kitaifa, Wazo Mwang’onda, ame miradi hiyo inalenga kuboresha huduma za kijamii.

Akiweka jiwe la Msingi katika mradi wa Barabara ya Maswi ,Pugu Kazimzumbwi yenye urefui wa kilometa 0.55 ambayo ujenzi wake ymagharimu sh. milioni 650, Mwang’onda alipongeza uongozi wa Wilaya ya Kisarawe kwa kuzingatia viwango vilivyo elekezwa na thamani ya fedha.

“Mwenge wa Uhuru umekagua na kupitia taarifa za ujenzi wa barabara hii. Barabara imekidhi vigezo hivyo Mwenge wa Uhuru umeridhia kuzindua babara hii,”amesema Mwang’onda.

Barabara hiyo iliyopo kitongoji cha Bomani ipo chini ya Wakala wa Barabara Mijini na Vijijini(TARURA).

Aidha Mwenge wa Uhuru umeweka jiwe la msingi na kufungua Mradi wa wa kitengo cha huduma za kibingwa za macho katika Hospitali ya Wilaya Kisarawe.

Mwang’onda, amepongeza hatua ya Wilaya ya Kisarawe kutoa huduma za kibingwa za machona kueleza dhamira ya Rais Dk. Samia ni kusogeza huduma bora za afya kwa wananchi.

Pia Mwenge wa Uhuru 2026 umezindua mradi wa kikundi cha vijana walionufaika na mkopo wa sh. milioni 35 za Halmashauri Wilaya ya Kisarawe.

“Rais Dk. Samia, ameelekeza vikundi vya vijana, wanawake na watu wenye ulemavu wakopeshwe fedha hizi. Vijana hawa wamekopa fedha na wameanzisha shughuli hii ya uselemala. Mwenge wa Uhuru umefurahishwa na hatua hii,”amesema.

Ametoa wito kwa vijana, wanawake na wenye ulemavu kuunda vikundi na kutumia fursa hiyo ya kukopa fedha halmashauri kujiinua kiuchumi.

Mradi mwingine uliomulikwa na Mwenge wa Uhuru ni Kiwanda cha Saruji cha Lucky Cement ambapo Mwang’onda alisema uwekezaji huo ni matunda ya utunzaji wa amani iliyopo nchini.

“Bila amani taifa haliwezi kuwa na uwekezaji mkubwa kama huu. Tuendelee kulinda amani ili kuvuta wawekezaji wengine kama hawa,”amesema.

Pia Mwenge wa Uhuru umeweka jiwe la msingi katika mradi wa upanuzi wa Mradi wa Maji wa Msanga kwenda vijiji vya Bembeleza na Chole.

Mradi huo uliogharimu sh. milioni 441 unatekelezwa na Wakala wa Majisafi Vijijini (RUWASA) na unatarajia kuondoa kero ya uhaba wa maji katika vijiji hivyo ukihusisha ujenzi wa tanki linalo chukua lita 90,000.

“Mwenge wa Uhuru umefurahishwa na utekelezaji wa mradi huu muhimu wa maji. Dhamira ya Rais Dk. Samia ni kuhakikisha maji safiyanapatikana hasa katika maeneo ya vijijini. Wito wangu wananchi wautunze mradi huu ili uwanufaishe,”amesema Mwang’onda.

Aidha Mwenge wa Uhuru umekagua mradi wa matumizi ya nishati safi na kupokea taarifa ya klabu ya mapambano ya rushwa katika Sekondari Menoromango katika Kijiji cha Menoromango, Kitongoji cha Kazimzumbwi.

Pia ulizindua mradi wa ujenzi wa madarasa mawili yaliyojengwa katika Shule ya Sekondari Kisarawe.

Awali akiwasilisha taarifa mbele ya Kiongozi wa Mbio za Mwenge, Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe, Petro Magoti, alisema ulipitia, kukagua na kuweka mawe ya msingi katika miradi saba ya maendeleo yenye thamani ya jumla y ash.bilioni 13.3.

Magoti, amesema Kisarawe inapiga hatua kubwa ya maendeleo hivyo kumshukuru Rais Dk. Samia kwa kuelekeza fedha nyingi za miradi zilizo gusa kila sekta, hususam elimu, afya, miundombinu ya barabara, maji, uwezeshaji wananchi kiuchumi na utalii.







Katibu Mkuu wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika  (CAF), Bw. Samson Adamu, amefanya kikao maalum na Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Hamis Mwinjuma, pamoja na Waziri wa Michezo wa Kenya Mhe. Salim Mvurya, Waziri wa Michezo wa Uganda Mhe. Peter Ongoing, na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Bw. Methusela Ntonda, ambapo kwa pamoja wamejadili hatua mbalimbali za maandalizi ya mashindano ya AFCON 2027.

Katika kikao hicho kilichofanyika Aprili 23, 2026 Kampala Uganda, viongozi hao wamepitia masuala muhimu yanayohusu maandalizi ya miundombinu, uratibu wa kamati za maandalizi, usalama, pamoja na mikakati ya kuhakikisha kuwa mashindano hayo yanafanyika kwa viwango vya kimataifa.

Mkutano huo ni mwendelezo wa jitihada za pamoja za Tanzania, Kenya na Uganda, nchi wenyeji wa mashindano hayo, katika kuhakikisha AFCON 2027 ambayo inatarajiwa kufanyika kuanzia Juni 19 hadi Julai 18, 2027 inafanikiwa na kuwa miongoni mwa mashindano bora zaidi kuwahi kufanyika barani Afrika.

Aidha, mkutano huo ulihudhuriwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Mashindano ya AFCON (Tanzania) Bw. Leodgar Tenga, pamoja na Marais wa mashirikisho ya mpira wa miguu wa mataifa wenyeji; Bw. Wallace Karia (Tanzania), Bw. Moses Magogo (Uganda), na Bw. Hussein Mohamed (Kenya).













Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, ameishauri Wizara ya Mambo ya Ndani kuimarisha mfumo wa utoaji wa viza kwa njia ya kidigitali ili huduma hiyo ipatikane kwa haraka kwa wageni wanaoingia nchini.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, tarehe 24 Aprili 2026, alipokutana na Waziri wa Mambo ya Ndani wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Patrobas Katambi, aliyefika Ikulu Zanzibar kwa ajili ya kujitambulisha.

Rais Dkt. Mwinyi amesema kuwa kwa muda mrefu kumekuwepo na tatizo la upatikanaji wa viza kupitia mfumo wa mtandao (online), jambo linalolalamikiwa na watalii wengi wanaoingia nchini na kusababisha kutumia muda mrefu kupata huduma hiyo katika viwanja vya ndege.

Amefahamisha kuwa hatua hiyo itaongeza ufanisi na kudhibiti upotevu wa fedha unaotokana na matumizi ya fedha taslimu. 

Amesisitiza kuwa kuwepo kwa mfumo wa kidigitali ni suala la lazima katika utoaji wa viza, na kuitaka Wizara kuchukua hatua za haraka kuondoa tatizo hilo.

Aidha, Rais Dkt. Mwinyi amesema kuwa suala jingine linalopaswa kupewa kipaumbele na Idara ya Uhamiaji ni uwajibikaji katika viwanja vya ndege, pamoja na kuimarisha utoaji wa huduma kwa haraka kwa kuwa na nguvu kazi ya kutosha muda wote na kuwajibika kwa ufanisi zaidi.

Sambamba na hilo, Rais Dkt. Mwinyi amesisitiza kwa Jeshi la Polisi kuimarisha usalama katika maeneo ya utalii ili kudhibiti matukio ya uhalifu, pamoja na kuongeza juhudi za kufanya uchunguzi wa haraka pale matukio yanapotokea na kuweka utaratibu mzuri wa utoaji wa taarifa kwa umma.

Akizungumzia suala la usalama barabarani, amesema juhudi za ziada zinahitajika kuimarisha utekelezaji wa sheria za usalama barabarani kutokana na kutofuatwa kikamilifu kwa sheria hizo, hali inayochangia ongezeko la ajali za barabarani. 

Pia amesisitiza kuimarishwa kwa juhudi za kupambana na udhalilishaji wa kijinsia, tatizo alilolieleza kuwa ni kubwa hapa nchini.

Naye Waziri wa Mambo ya Ndani, Mhe. Patrobas Katambi, amemuhakikishia Rais Dkt. Mwinyi kuwa Wizara hiyo itaendelea kutekeleza majukumu yake kwa utii na uaminifu, kwa kuzingatia Katiba, sheria na sera za nchi, na ameahidi kuyapokea na kuyafanyia kazi maelekezo yote yaliyotolewa kama dira ya utekelezaji.











Viongozi wa vyama vya ushirika mkoani Geita wametakiwa kusimamia maadili kwa dhati ili kuhakikisha wadau, hususan wakulima wadogo, wanapata haki na stahiki zao kwa wakati. 

Agizo hilo limetolewa na Mkuu wa Wilaya ya Geita, Mhe. Hashim Komba, kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mhe. Martin Shigela, wakati wa kilele cha Jukwaa la 4 la Maendeleo ya Ushirika mkoani humo lililofanyika Aprili 22 mwaka huu.

Katika hotuba yake, Mhe. Komba amezitaka AMCOS mbalimbali kuhakikisha zinawalipa wadau madeni yao kila msimu unapoisha. Alibainisha kuwa kwa sasa halmashauri pekee zinadai takribani Shilingi Milioni 50 huku wanunuzi wakidai takribani Shilingi Milioni 100, hali ambayo alionya kuwa inaweza kuhatarisha uhakika wa soko la mazao na bidhaa mbalimbali mkoani humo ikiwa hatua hazitachukuliwa.

Kwa upande wake, Mrajisi Msaidizi wa Vyama vya Ushirika mkoani Geita, Bi. Doreen Mwanry, amewahimiza wananchi ambao bado si wanachama kujiunga na ushirika ili kupata huduma sahihi. 

Alieleza kuwa mkoa una jumla ya vyama 629 vyenye wanachama 5,084, na tayari vyama hai 304 vimeshasajiliwa kwenye Mfumo wa kusajili na kusimamia vyama vya ushirika nchini (MUVU).

Naye Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa, Dkt. Elfas Msenya, ametoa wito kwa AMCOS kusimamia taratibu za mfumo wa stakabadhi ya ghala kutokana na mafanikio makubwa yaliyopatikana kwenye zao la dengu msimu uliopita. 

Alisisitiza kuwa kufuata taratibu hizo kutawezesha mazao yote kuingizwa kwenye mfumo na kuhakikisha wakulima wanapata faida kulingana na bei elekezi zilizotangazwa. 









Mwenyekiti wa Chama cha Wanawake Wachimbaji Madini Tanzania (TAWOMA) Mkoa wa Dodoma, Jesca Nsamba, amesema wanawake wanaendelea kunufaika na mageuzi yanayofanyika katika sekta ya madini, huku akitoa pongezi kwa serikali kwa mchango wake mkubwa katika kukuza sekta hiyo.

Ameyasema hayo leo jijini Dodoma wakati wa kongamano la fursa na mageuzi kwa wanawake katika sekta ya madini, ambapo amebainisha kuwa wanawake wamekuwa miongoni mwa wanufaika wakubwa wa juhudi hizo.

Ameeleza kuwa licha ya msaada unaotolewa na serikali, wanawake wamekuwa wakionyesha juhudi binafsi kwa kuhakikisha wanatekeleza majukumu yao kwa bidii bila kusubiri kufanyiwa kila kitu na  kupitia TAWOMA, wameendelea kuweka mikakati ya kuwainua wanawake ili waweze kunufaika kikamilifu na fursa zilizopo katika sekta ya madini nchini.

Nsamba amesisitiza kuwa si muda mrefu tangu wanawake waanze kushiriki katika shughuli za madini, ambazo hapo awali zilionekana kuwa ni kazi za wanaume pekee, hata hivyo kwa sasa mafanikio yao yanaonekana wazi, huku wanawake wengi wakijitokeza na kushiriki kikamilifu katika shughuli hizo na kuchangia ukuaji wa uchumi wa taifa.

Amezitaja changamoto zinazowakabili wanawake katika sekta hiyo kuwa ni pamoja na ukosefu wa mitaji na vifaa, akitoa wito kwa wadau na wafadhili kuongeza msaada zaidi ili kuwawezesha kufikia malengo yao, pia amewahimiza wanawake kuwa na ujasiri na kujiamini, akieleza kuwa wana uwezo mkubwa wa kufanikiwa katika sekta ya madini.




Na Pamela Mollel,Arusha 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, Riziki Shemdoe amesema taasisi ya mpango wa usalama barabarani (TARSI) ina mchango mkubwa katika kuimarisha taaluma ya uhandisi na kupunguza ajali za barabarani kupitia utoaji wa mafunzo kwa wataalamu nchini.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya siku tatu kwa wahandisi kuhusu usalama barabarani, Shemdoe alisisitiza kuwa serikali inaona umuhimu wa wahandisi kuendelea kupata mafunzo ya mara kwa mara ili kuongeza ufanisi katika ubunifu na usimamizi wa miundombinu salama.

Alieleza kuwa juhudi hizo ni sehemu ya mkakati mpana wa serikali wa kuhakikisha barabara zinakuwa salama zaidi kwa watumiaji wote, ikiwa ni pamoja na madereva, waendesha pikipiki na watembea kwa miguu.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa TARSI, Maliki Barongo, alisema taasisi hiyo imejikita katika kutoa elimu na tafiti zinazolenga kupunguza ajali za barabarani, huku akihimiza wadau kushirikiana kwa karibu ili kufikia malengo hayo.

Naye Mkuu wa Kitengo cha Utafiti kutoka Taasisi ya Mifupa (MOI), Dkt. Joel Bwemelo, alieleza umuhimu wa kuchukua tahadhari na kuzingatia kanuni za usalama barabarani ili kupunguza athari za ajali zinazoweza kuepukika.

Aidha, Laurent Maganga kutoka Norplan Tanzania alipendekeza elimu ya usalama barabarani iingizwe katika mitaala ya uhandisi, akisema hatua hiyo itasaidia kuzalisha wahandisi wenye uelewa mpana wa masuala ya usalama tangu wakiwa vyuoni.

Mafunzo hayo yamewakutanisha wahandisi kutoka maeneo mbalimbali nchini, yakilenga kubadilishana uzoefu na mbinu bora za kitaalamu zitakazochangia kuboresha ubora wa barabara pamoja na kupunguza ajali zinazotokana na mapungufu ya miundombinu.








Top News