SERIKALI imesema Mwitikio wa vijana kutaka kukopeshwa fedha kwaaji li ya kuanzisha biashara umekuwa mkubwa na wa kutia moyo baada ya baadhi ya masharti magumu yaliyokuwa yakiwashinda vijana kuondolewa.
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa programu ya Kitaifa ya utoaji wa mikopo kupitia programu ya billioi 200 chini ya mfuko wa maendeleo ya vijana leo 9 Julai 2026,Jijini Arusha, Waziri wa nchi ofisi ya Rais Vijana, Joel Nananuka amesema miongoni mwa changamoto zilizokuwa zikilalamikiwa ni riba kubwa kwa wakopaji.
“Riba ilikuwa ni changamoto, na Sasa riba imeondolewa mtu akishapata mikopo na kulipa bima basi atapata mikopo wake, pia kulikuwa na changamoto ya mikopo kurejesha mapema, tunataka mtu akipata fedha aanze kufanyia kazi ndipo aanze kurejesha, mwongozo mpya ni kwamba watakaa na mkopo kwa miezi mitatu kabla ya kuanza kurejesha,” amesema.
Amesema changamoto nyingine iliyofanyiwa mabadiliko ni mtu mmoja mmoja kupata fedha kama alivyoomba badala ya kuwa katika kikundi ndio update fedha hizo kama ilivyokuwa hapo awali.
“ Ilikuwa fedha zinatolewa kwa vikundu pekee na sio mtu mmoja mmoja lakini sasa hivi kama tulivyoagizwa na Mheshimiwa Rais Samia tuondoe vikwazo vyote, basi awamu hii vijana wengi watapata mkopo Kwa namna alivyoomba bila kupitia kikundi,” amesema.
Amesema baada ya kutatuliwa Kwa changamoto hizo, jumla ya maombi 30,384 yalipokelewa kutoka maeneo mbalimbali nchini yakihusisha sekta za kilimo, mifugo, uvuvi, viwanda vidogo, biashara, ubunifu, teknolojia na huduma mbalimbali.
“ Takwimu hizi zinaonesha wazi kuwa vijana wa Tanzania si wavivu kama ambavyo wakati mwingine imekuwa ikidaiwa;
badala yake, wanahitaji mazingira yanayowapa fursa ya kuonesha uwezo wao,” amesema Nanauka na kuongeza:
“Baada ya mchakato wa kina wa tathmini uliozingatia vigezo vilivyowekwa, kwa awamu ya kwanza tunaenda kuwezesha miradi ya vijana yenye thamani ya Shilingi Bilioni 8 kupitia Mfuko wa Maendeleo ya vijana unapojaribiwa na Ofisi ya Rais - Maendeleo ya vijana,” amesema.
Amesema katika uzinduzi wa programu hiyo, katika Mkoa wa Arusha mikopo ya shilingi milioni 730 itatolewa ambapo milioni 500 zitaenda katika utafiti na utengenezaji wa dawa za binadamu, Milioni 130 zitaenda katika kiwanda cha vijana kinachotengeneza chaki zisizotoa vumbi na milioni 100 zitaenda kwa viundi vya Mama na Baba Lishe.
“ Hii ni hatua ya mwanzo ambayo itaendelea kupanuliwa kadri fedha zitakavyopatikana na tathmini za utekelezaji zitakavyoendelea kuonesha mafanikio,” amesema.
Amesema fedha hizo ni za uwekezaji wa Taifa kwa vijana wake na kwamba Serikali imewaamini na imeamua kuwekeza kwa vijana kwa matarajio kwamba watazitumia kuongeza uzalishaji, kupanua biashara, kuanzisha viwanda vidogo, kuongeza thamani ya bidhaa na kuzalisha ajira kwa vijana wengine.
“Napenda kuwasisitiza kuwa mafanikio ya programu hii hayatapimwa kwa kiwango cha fedha kilichotolewa, bali kwa matokeo yatakayopatikana. Tunataka kuona biashara zenye tija, ongezeko la mapato ya kaya, ajira mpya, ukuaji wa kampuni za vijana na mchango mkubwa wa sekta ya vijana katika pato la Taifa, “ amesema na kuongeza:
“Hivyo basi, nawasihi mtumie fedha hizi kwa malengo yaliyokusudiwa; wekeni mifumo mizuri ya usimamizi wa fedha; tunzeni kumbukumbu za biashara zenu; zingatieni misingi ya utawala bora wa biashara; na hakikisheni mnarejesha mikopo kwa wakati. Nidhamu ya fedha ndiyo msingi wa mafanikio ya biashara yoyote duniani.” Amesema.
Awali Mkuu wa Mkoa wa Arusha CPA Amos Makala amesema vijana wa Arusha wanajitambua na hawachezi na fursa na kwamba Kwa juhudi wanazoendelea nazo ana uhakika kesho yao itakuwa njema.
Mwakilishi wa benki ya CRDB, Meneja wa Benki hiyo tawi la Meru Arusha, Haika Mawalla amesema CRDB Bank inajivunia kuaminiwa na Serikali kupewa jukumu la kusimamia utekelezaji wa mpango huo wa uwezeshaji wa vijana nchini kote.
“ Hili ni jukumu kubwa na tunalipokea kwa uzito, uadilifu na uwajibikaji. Tumejipanga kuhakikisha huduma hii inawafikia vijana wengi iwezekanavyo kwa uwazi, ufanisi na weledi,” amesema.
Amesema mbali na kutoa mikopo, CRDB itaendelea kuwajengea vijana uwezo kupitia elimu ya fedha, usimamizi wa biashara na matumizi sahihi ya mikopo na kwamba wanaamini kuwa mchanganyiko wa mtaji, maarifa na nidhamu ya fedha ndio msingi wa mafanikio ya biashara na ujasiriamali endelevu.
“Tunawasihi vijana wote kuitumia fursa hii kwa ubunifu, uwajibikaji na uaminifu. Mikopo hii ni chachu ya maendeleo; itumike kuanzisha na kukuza miradi yenye tija, kuongeza ajira na kuinua uchumi wa familia na Taifa kwa ujumla,” amesema.



.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)



.jpeg)

.jpeg)





.jpeg)










.jpeg)
.jpeg)






.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)









.jpg.jpeg)

