Na Beda Msimbe,TBN, Moscow. 

 Urusi imesema taifa hilo litafungua fursa lukuki kwa taifa la Tanzania kwa manufaa ya pande zote mbili.

Aidha taifa hilo lenye miradi 70 yenye thamani ya dola za Marekani milioni434.22 ikiwa imewezesha ajira 3018 tanzania limesema kuwa litatangaza fursa hizo katika mkutano wa uchumi wa kimataifa kesho kutwa.

Akizungumza na waandishi wa habari baada ya kikao chake na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kiongozi wa Urusi Vladimir Putin amesema Urusi imekuwa ikifuatilia kwa makini mageuzi yanayofanyika nchini tanzania na wanaona inavyokua.

Amesema amekuwa na mazungumzo yenye manufaa makubwa kwa jamii ya pande zote mbili na kuahidi kuendelea na ushirikiano na Tanzania. Naye rais Samia amesema kuwa ziara yake katika Shirikisho la Urusi ina umuhimu mkubwa wa kihistoria kwake binafsi na kwa taifa la Tanzania kwa ujumla.

“Ziara yangu ina umuhimu wa pekee wa kihistoria kwangu binafsi na kwa nchi yangu. Imepita zaidi ya nusu karne tangu kufanyika kwa ziara ya mwisho ya kiserikali ya Tanzania nchini Urusi. Hivyo, kwangu hii ni safari ya kihistoria sana kuja Urusi kujadili masuala mbalimbali ya ushirikiano wa pande mbili, pamoja na maendeleo endelevu kwa wananchi wetu. Kwa niaba yangu na wananchi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, napenda kutoa shukrani zetu za dhati kwa mwaliko huu,” alisema Rais Samia.

Aidha, Rais Samia alikumbusha mchango mkubwa wa Urusi katika harakati za Tanzania za kupigania uhuru na kumpongeza Rais Putin kwa maadhimisho ya miaka 81 ya Ushindi katika Vita Kuu ya Pili ya Dunia yaliyofanyika Mei 9 mwaka huu.

Rais Samia aliwasili Moscow kwa ziara yake ya kwanza nchini Urusi, ambayo pia ni ziara ya kwanza ya kiongozi wa Tanzania nchini humo katika kipindi cha zaidi ya miaka 50, kwa ajili ya mazungumzo na Rais Putin.

Viongozi hao kwa mujibu wao walijadili masuala mbalimbali yanayohusu kuimarisha zaidi uhusiano wa kirafiki na ushirikiano kati ya nchi hizo mbili. Vilevile, walibadilishana mawazo kuhusu masuala muhimu yanayohusu ajenda za kimataifa na kikanda.






Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiweka Shada la maua katika Kaburi la Askari Asiyejulikana (Tomb of the Unknown Soldier) pembezoni mwa Ukuta wa Ikulu ya Kremlin Jijini Moscow nchini Urusi, tarehe 03 Juni, 2026.


Na Beda Msimbe, TBN, Moscow

Kengele kubwa iliyogongwa mara tisa huku bendi ya jeshi ikiongoza nyimbo za maombolezo, Rais Dk. Samia Suluhu Hassan majira ya saa tano na dakika 23 aliweka shada la maua katika kaburi la Askari Asiyefahamika mjini Moscow, Urusi.

Baada ya shughuli hiyo ya uwekaji wa shada la maua katika eneo ambalo moto huwaka daima kama kumbukumbu ya wapiganaji wa Urusi waliopoteza maisha katika Vita Kuu ya Pili ya Dunia, gadi tatu za heshima zilipita kwa mwendo wa haraka kutoa salamu za heshima kwa Rais Samia, sambamba na kupigwa kwa wimbo wa Taifa wa Tanzania.

Nidhamu ya askari waliokuwa katika uwanja huo ilivutia wengi, ambapo walionekana kusimama kwa umakini mkubwa bila kutikisika katika maeneo yao ya ulinzi. Aidha, ubadilishanaji wa gadi pamoja na mwendo wa pole uliomsindikiza Rais Samia kuelekea eneo la uwekaji wa shada la maua viliongeza hadhi na mvuto wa tukio hilo la kihistoria.

Rais Samia ambaye yupo nchini Urusi kwa ziara ya kiserikali, baadaye alikutana na mwenyeji wake, Rais wa Urusi Vladimir Putin, kwa mazungumzo yanayolenga kuimarisha uhusiano na ushirikiano kati ya Tanzania na Urusi.

Zaidi ya maofisa 300 wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) wamepata nafasi ya masomo nchini Urusi katika ngazi za shahada ya kwanza na shahada ya pili.

Maofisa hao wamekuwa wakipatiwa mafunzo katika maeneo mbalimbali ikiwemo mapambano dhidi ya ugaidi, sayansi na teknolojia, mafunzo ya kijeshi, operesheni za ulinzi wa amani, ununuzi na uhifadhi wa silaha pamoja na namna ya kukabiliana na majanga.

Tanzania na Urusi zinaendelea kuimarisha ushirikiano wa kijeshi kwa kuzingatia makubaliano ya ushirikiano wa kijeshi yaliyosainiwa mwaka 2016 pamoja na makubaliano ya ushirikiano wa kifundi wa kijeshi ya mwaka 2018.

Kwa upande mwingine, Tanzania inaendelea kushuhudia ukuaji wa uchumi unaokadiriwa kufikia asilimia 5.5 mwaka 2024 na matarajio ya kufikia asilimia 6 mwaka huu, huku Serikali ikiendelea kusimamia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Kutokana na hali hiyo, ziara ya Rais Samia nchini Urusi inatarajiwa kufungua fursa mpya za kiuchumi kupitia ajira, biashara, uwekezaji pamoja na ushirikiano wa kiteknolojia na kijeshi kati ya mataifa hayo mawili.



NAIBU Kamishna wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Zanzibar, Saleh Haji Pandu, amesema kuwa Mfumo wa Pamoja wa Uondoshaji wa Shehena Maeneo ya Forodha Zanzibar (The Zanzibar Single Window) utachangia kurahisisha mazingira ya biashara Zanzibar na kupunguza urasimu unaowakabili wafanyabiashara.

Akizungumza kwa niaba ya Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Yusuph Mwenda, wakati wa uzinduzi wa mradi huo uliofanyika katika hoteli ya Madinat Al Bahr Mazizi Mweni, Zanzibar, Pandu alisema kuwa mfumo huo utaimarisha utoaji wa huduma kwa kuwezesha taasisi mbalimbali za serikali kufanya kazi kwa pamoja kupitia jukwaa moja la kidijitali.

Alifafanua kuwa kabla ya kuanzishwa kwa mfumo huo, wafanyabiashara walilazimika kutembelea taasisi mbalimbali ili kukamilisha taratibu za uingizaji wa bidhaa na biashara, hali iliyosababisha ucheleweshaji wa huduma pamoja na kuongeza gharama za uendeshaji.

Aidha, alisema kuwa uzinduzi wa mfumo huo ni hatua muhimu katika utekelezaji wa mageuzi ya kidijitali yanayolenga kuimarisha ushirikiano wa taasisi za serikali, kuboresha mazingira ya biashara na kuchochea maendeleo ya uchumi.

“Tutakapokuwa na mifumo kama hii tutapunguza kiwango cha udanganyifu, kuongeza ukusanyaji wa mapato, na serikali yetu itanufaika zaidi katika kutekeleza miradi ya maendeleo,” alisema Pandu.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya TEHAMA kutoka Huduma za Forodha Korea, Kim Ki-dong, ambaye taasisi yake inasaidia katika ujenzi wa mfumo huo, alisema kuwa uboreshaji wa mifumo ya kidijitali utaimarisha utendaji wa Idara ya Forodha Zanzibar na Tanzania kwa ujumla.

Aliongeza kuwa Taasisi ya Huduma za Forodha Korea (Korea Customs Service - KCS) itaendelea kutoa ushirikiano wa karibu kwa Idara ya Forodha Tanzania katika ujenzi wa mifumo ya kisasa itakayoboresha utendaji wa forodha, hususan katika matumizi ya teknolojia za kielektroniki.

Naye Rais wa Jumuiya ya Mawakala wa Forodha Zanzibar (ZFB), Omar Hussein Mussa, alisema kuwa kwa sasa mawakala wa forodha wanakabiliwa na changamoto ya ucheleweshaji wa uondoshaji wa mizigo kutokana na kulazimika kufika katika zaidi ya taasisi 14 ili kukamilisha taratibu zinazohitajika.

Alisema kuwa utekelezaji wa Mfumo wa Pamoja wa Uondoshaji wa Shehena Maeneo ya Forodha Zanzibar (The Zanzibar Single Window) utarahisisha mchakato huo kwa kuwawezesha mawakala na wafanyabiashara kukamilisha taratibu kwa haraka zaidi, kwa gharama nafuu na bila ya usumbufu.

“Kwa sasa tunalazimika kutembelea zaidi ya taasisi 14 na kufuatilia nyaraka mbalimbali ili kutoa shehena forodhani. Mfumo huu ukianza kufanya kazi utarahisisha shughuli hizo na kuendana na mazingira ya kisasa ya biashara duniani,” alisema Omar.

Mfumo wa Pamoja wa Uondoshaji wa Shehena Maeneo ya Forodha Zanzibar (The Zanzibar Single Window) unatarajiwa kuwa nyenzo muhimu katika kuharakisha utoaji wa huduma za biashara, kuongeza uwajibikaji katika usimamizi wa kodi na mapato ya serikali, pamoja na kuboresha mazingira ya uwekezaji na biashara Zanzibar.




Naibu Waziri wa Maji, Nishati na Madini Zanzibar, Mhe. Seif Kombo Pandu kushoto na Mkurugenzi wa Airtel Money Tanzania, Bw. Andrew Rugamba kulia wakipeana mikono na kubadilishana zawadi wakati wa kuzindua rasmi ushirikiano wa kimkakati wa "Airtel Money na ZECO – Tukuza Kidigitali" unaolenga kurahisisha malipo ya umeme visiwani humo. Uzinduzi huo umefanyika leo Zanzibar, Juni 2026.
Naibu Waziri wa Maji, Nishati na Madini Zanzibar, Mhe. Seif Kombo Pandu, akihutubia wakati wa uzinduzi rasmi wa ushirikiano wa kimkakati wa "Airte
Mkurugenzi wa Airtel Money Tanzania, Bw. Andrew Rugamba, akizungumza wakati wa uzinduzi rasmi wa ushirikiano wa kimkakati wa "Airtel Money na ZECO – Tukuza Kidigitali.", akisisitiza dhamira ya Airtel ya kuendelea kuleta urahisi na ufanisi wa huduma za kifedha kwa wananchi wa Zanzibar.

*Ushirikiano wa Airtel Money na ZECO kurahisisha malipo ya umeme wa TUKUZA visiwani humo.
*Waziri wa Nishati apongeza hatua hiyo akitaja kuwa itachochea Uchumi wa Bluu na maendeleo ya kidigitali.
*Benki ya PBZ yajipanga kuhakikisha ukwasi wa kutosha kwa mawakala ili kufanikisha miamala.

Zanzibar, Juni 2, 2026 
KAMPUNI ya mawasiliano ya Airtel Tanzania, kupitia huduma yake ya Airtel Money, imeingia mkataba wa kimkakati na Shirika la Umeme Zanzibar (ZECO) kupitia mpango uitwao “Airtel Money na ZECO – Tukuza Kidigitali”.

Ushirikiano huu unalenga kuleta mageuzi makubwa katika ununuzi na malipo ya nishati ya umeme wa mfumo wa TUKUZA visiwani humo.

Kupitia mfumo huo mpya, wateja wa Airtel sasa wataweza kununua umeme wa TUKUZA kwa haraka, usalama na urahisi mkubwa kupitia simu zao za mkononi, mahali popote na wakati wowote, bila kulazmika kufika vituoni.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Naibu Waziri wa Maji, Nishati na Madini Zanzibar, Mhe. Seif Kombo Pandu, ameupongeza ushirikiano huo akitaja kuwa ni hatua kubwa kuelekea uchumi wa kidigitali na kuboresha utoaji wa huduma za umma.

“Ushirikiano huu unaonesha dhamira yetu ya kuhakikisha wananchi wanapata huduma za kisasa na zinazofikika kwa urahisi kupitia teknolojia. Umeme ni kichocheo kikuu cha uchumi wetu, ukisaidia sekta za utalii, afya, elimu, viwanda, pamoja na biashara ndogo na za kati (SMEs). Kila hatua inayorahisisha upatikanaji wake inachangia moja kwa moja katika maendeleo ya Zanzibar,” alisema Mhe. Pandu.

Naibu Waziri aliongeza kuwa mpango huo unaenda sambamba na malengo ya Sera ya Nishati Zanzibar ya mwaka 2025 pamoja na Mpango wa Maendeleo ya Nishati wa Miaka 15 (2025–2040), unaolenga kuimarisha usalama wa nishati na kupunguza gharama za uendeshaji.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Airtel Money Tanzania, Bw. Andrew Rugamba, alisema: “Kupitia ushirikiano huu na ZECO, wateja wa TUKUZA sasa wanaweza kurejesha nishati ya umeme kwenye makazi au biashara zao ndani ya sekunde chache tu. Huu ndio urahisi na ufanisi tunaotaka kuuleta kwa wananchi wa Zanzibar.”

Bw. Rugamba alibainisha kuwa, kupitia kampeni ya “Airtel Kila Kona”, kampuni hiyo imeendelea kuwekeza kwa kiasi kikubwa Zanzibar. Uwekezaji huo ni pamoja na kufungua vituo vipya vya huduma katika Mkoa wa Mjini Magharibi (eneo la ZSSF Mbweni) na kituo kikubwa cha kisasa katika Jengo la Muzammil, Mlandege.

Naye Meneja Mipango na Biashara wa Shirika la Umeme Zanzibar (ZECO) Bi. Aisha Omary, alifafanua kuwa hatua hiyo ni sehemu ya mkakati wa shirika hilo wa kutumia ubunifu wa kidigitali kuondokana na mifumo ya kizamani ya utoaji huduma. “Huu siyo tu urahisi wa malipo, bali ni hatua kubwa ya kujenga mfumo wa nishati wenye ufanisi na unaowajumuisha wananchi wengi zaidi,” alisema Bi. Omary.

Katika kuhakikisha huduma hiyo inasafiri bila vikwazo, Mkurugenzi Mkuu wa Benki ya Watu wa Zanzibar (PBZ), Bw. Arafat Ally Haji, aliahidi kuwa benki hiyo itahakikisha mawakala wote wa Airtel Money visiwani humo wanakuwa na ukwasi (float) wa kutosha wakati wote.

“Kupitia ushirikiano wetu na Airtel, PBZ itahakikisha miamala yote, ikiwemo ununuzi huu wa umeme wa TUKUZA, inafanyika kwa haraka na ufanisi wa hali ya juu bila kukwama kwa kukosekana kwa fedha mtandaoni,” alisisitiza Bw. Arafat.

Uzinduzi huu wa mpango wa “Airtel Money na ZECO – Tukuza Kidigitali” unadhihirisha nguvu ya ushirikiano kati ya sekta ya umma na binafsi (PPP) katika kuongeza ujumuishi wa kifedha na kuharakisha maendeleo ya kijamii na kiuchumi nchini.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amekutana na mwanazuoni na mhamasishaji wa dhana ya Utalii Halali Duniani, Bw. Ismail Bullock kutoka Dubai.

Mazungumzo hayo yamefanyika leo, tarehe 03 Juni 2026, Ikulu Zanzibar, alipofika kujitambulisha pamoja na ujumbe alioambatana nao kutoka Taasisi ya Samia Foundation.

Rais Dkt. Mwinyi amesifu kazi nzuri anayofanya mwanazuoni huyo katika kutangaza na kuhamasisha Utalii Halali katika mataifa mbalimbali duniani, na kuahidi kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inaridhishwa na inaunga mkono juhudi zake za kukuza na kuendeleza utalii unaofuata misingi ya Kiislamu.

Aidha, amesema Zanzibar itaendelea kujifunza zaidi kupitia uhamasishaji na mafunzo anayoyatoka kwa wadau wa sekta ya utalii, na kumshauri kuendelea na jukumu hilo kutokana na manufaa makubwa yanayopatikana kwa nchi na wadau wa utalii katika kufahamu njia bora na sahihi za kutekeleza Utalii Halali (Halal Tourism).

Dkt. Mwinyi amepongeza hatua ya Bw. Ismail Bullock ya kuchapisha na kusambaza nakala za Kitabu Kitakatifu cha Qur'an kilichotafsiriwa kwa lugha ya Kiingereza, akieleza kuwa ni hatua muhimu inayoweza kuwasaidia wadau wengi zaidi kuelewa dhana ya Utalii Halali, na kumhakikishia ushirikiano zaidi.

Naye mwanazuoni Bw. Ismail Bullock amesema dhamira yake kuu ni kuona dhana ya Utalii Halali inaeleweka na kutekelezwa katika mataifa mbalimbali duniani. Amesema tayari dhana hiyo imeendelea kupata umaarufu mkubwa katika nchi nyingi duniani.

Bw. Ismail Bullock kwa sasa, yupo Zanzibar ambako anaendelea kutoa mafunzo kwa wadau wa sekta ya utalii kuhusu dhana ya Utalii Halali.







Jumla ya vijana 588 wanaonufaika na mpango wa ufadhili wa mafunzo ya ufundi stadi kwa vijana wa ‘NBC Wajibika Scholarship’ wameanza rasmi mafunzo yao katika vyuo vya VETA Kihonda mkoani Morogoro na VETA Mwanza, huku Benki ya NBC ikisisitiza dhamira yake ya kuendelea kuwekeza katika maendeleo ya rasilimali watu kama njia ya kuchochea ukuaji wa uchumi jumuishi nchini.

Mpango huo unatekelezwa kwa ushirikiano kati ya Benki ya NBC na Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA), ukiwa na lengo la kuwawezesha vijana kupata ujuzi unaowawezesha kujiajiri, kuajiriwa na hata kuwa waajiri, sambamba na kuunga mkono jitihada za Serikali za kujenga uchumi shindani unaotegemea nguvu kazi yenye ujuzi, ubunifu na tija.

Hafla ya uzinduzi wa utekelezaji wa mpango huo ilifanyika jana katika Chuo cha VETA Kihonda, ambapo wanafunzi 294 wanapatiwa mafunzo, huku idadi kama hiyo ikinufaika katika Chuo cha VETA Mwanza. Hafla hiyo ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa VETA wakiongozwa na Mkurugenzi wa VETA Kanda ya Mashariki, Bw. John Mwanja, aliyemwakilisha Mkurugenzi Mkuu wa VETA, Mkuu wa Chuo cha VETA Kihonda, Dkt. Ulimwengu Salumu, walimu, wanafunzi wanufaika pamoja na maofisa wa NBC wakiongozwa na Mkuu wa Idara ya Mawasiliano na Mahusiano kwa Umma, Bw. Godwin Semunyu.

Kupitia mpango huo, NBC imetoa ufadhili wa zaidi ya shilingi milioni 150 kwa ajili ya kugharamia mafunzo ya muda mfupi kwa vijana hao katika fani za Ufundi Umeme, Ufundi Bomba pamoja na Ubunifu, Ushonaji na Teknolojia ya Nguo.

Akizungumza katika hafla hiyo, Bw. Semunyu alisema kuwa uwekezaji wa NBC katika elimu ya ufundi stadi unalenga kuwawezesha vijana kujenga mustakabali wao wa kiuchumi na wakati huo huo kuchangia maendeleo ya taifa.

“Mbali na uwekezaji wetu katika sekta za afya, elimu na michezo, suala la ajira kwa vijana ni eneo muhimu tunalolipa kipaumbele. Takwimu zinaonesha kuwa zaidi ya asilimia 70 ya Watanzania wana umri wa chini ya miaka 35. Hii ni rasilimali kubwa inayohitaji kupewa maarifa na ujuzi ili iweze kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya uchumi wa nchi,” alisema.

Aliongeza kuwa ongezeko la wahitimu wanaoingia katika soko la ajira kila mwaka linaifanya elimu ya ufundi stadi kuwa mojawapo ya suluhisho muhimu katika kukuza ajira, ubunifu na kujitegemea kiuchumi.

“Tunaamini kuwa elimu ya ufundi stadi ni daraja muhimu la kuwawezesha vijana kujenga maisha yao kupitia ujuzi unaotambulika na unaohitajika katika soko la ajira la sasa. Ndiyo maana tunaendelea kuwekeza katika mipango yenye matokeo ya moja kwa moja kwa jamii,” aliongeza.

Aidha, aliwataka wanafunzi wanaonufaika na ufadhili huo kutumia kikamilifu fursa waliyoipata kwa kujifunza kwa bidii ili waweze kuhitimu wakiwa na maarifa, ujuzi na umahiri unaohitajika katika mazingira ya kisasa ya kazi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa VETA Kanda ya Mashariki, Bw. John Mwanja, aliipongeza NBC kwa mchango wake katika kuendeleza elimu ya ufundi stadi nchini, akisisitiza kuwa ushiriki wa sekta binafsi ni nyenzo muhimu katika kuhakikisha mafunzo yanayoandaliwa yanaendana na mahitaji halisi ya soko la ajira.

“Ushirikiano kati ya sekta binafsi na taasisi za mafunzo ni nguzo muhimu ya maendeleo ya taifa. Kupitia ushirikiano huo tunaweza kubaini mahitaji ya soko la ajira, kuboresha mazingira ya kujifunzia, kuongeza fursa za mafunzo kwa vitendo na kuimarisha uwezekano wa wahitimu kupata ajira au kujiajiri,” alisema.

Naye Mkuu wa Chuo cha VETA Kihonda, Dkt. Ulimwengu Salumu, alisema kuwa mafunzo hayo ya miezi mitano yalianza rasmi Mei 25 mwaka huu na yanajumuisha masomo ya nadharia pamoja na mafunzo kwa vitendo ili kuwajengea wanafunzi uwezo wa kufanya kazi katika mazingira halisi ya uzalishaji.

Alisema mbali na stadi za kitaaluma, wanafunzi hao pia wanapatiwa mafunzo ya ujasiriamali na stadi za maisha ili kuwawezesha kuanzisha na kusimamia biashara zao pamoja na kujenga mahusiano bora katika jamii.

“Tuna matarajio makubwa kuwa wahitimu wa programu hii watakuwa na uwezo wa kushindana katika soko la ajira, kujiajiri na kuchangia kikamilifu maendeleo ya uchumi wa taifa,” alisema Dkt. Ulimwengu.

Baadhi ya wanafunzi wanaonufaika na mpango huo walieleza shukrani zao kwa NBC, VETA na Serikali kwa kuwapatia fursa hiyo, wakisema mafunzo hayo yanakwenda kuwafungulia njia mpya za kutimiza ndoto zao za kujitegemea kiuchumi kupitia ujuzi wa ufundi stadi.

“Tunawasjukuru sana NBC kwa kubuni na kuona umuhimu wa program hii. Matarajio yetu baada ya kuhitimu ni kuanzisha shughuli zetu binafsi za uzalishaji mali, kujiajiri na hatimaye kuwaajiri vijana wengine katika jamii,” alisema mmoja wa wanufaika, Peter Lwana, kauli iliyoungwa mkono na wenzake Penina Nilanga, Fauzia Kassim na William Amon.

Mkurugenzi wa VETA Kanda ya Mashariki, Bw. John Mwanja (wa pili kushoto), Mkuu wa Idara ya Mawasiliano na Mahusiano kwa Umma wa Benki ya Taifa ya Biashara (NBC), Bw. Godwin Semunyu (wa tatu kushoto), na Mkuu wa Chuo cha VETA Kihonda, Dkt. Ulimwengu Salumu (wa tatu kulia) , walimu na wanafunzi, wakisikiliza maelezo kutoka kwa mwanafunzi wa kozi fupi ya Ufundi Bomba katika Chuo cha VETA Kihonda, William Amon (katikati), kuhusu mfumo wa kilimo cha umwagiliaji uliobuniwa na wanafunzi hao. William ni miongoni mwa vijana 588 wanaonufaika na mpango wa ufadhili wa mafunzo ya ufundi stadi kwa vijana unaojulikana kama NBC Wajibika Scholarship, unaotekelezwa na VETA kwa ufadhili wa NBC. Tukio hilo lilifanyika leo mkoani Morogoro wakati wa uzinduzi rasmi wa utekelezaji wa mpango huo.

Mkurugenzi wa VETA Kanda ya Mashariki, Bw. John Mwanja (Katikati) akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) wakati wa hafla fupi ya uzinduzi wa utekelezaji wa mpango wa ufadhili wa mafunzo ya ufundi stadi kwa vijana unaojulikana kama ‘NBC Wajibika Scholarship’, kwa tawi la VETA Kihonda Morogoro. Mradi huo unaotekelezwa na na Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) kwa ufadhili wa NBC. Wengine ni Mkuu wa Idara ya Mawasiliano na Mahusiano kwa Umma wa Benki ya Taifa ya Biashara (NBC), Bw. Godwin Semunyu (kushoto), na Mkuu wa Chuo cha VETA Kihonda, Dkt. Ulimwengu Salumu (kulia).

Akizungumza katika hafla hiyo, Bw. Semunyu (katikati) alisema kuwa kupitia mpango huo NBC inalenga kuwawezesha vijana kupata ujuzi utakaowapa uwezo wa kujiajiri, kuajiriwa na hata kuwaajiri wengine, hivyo kuchangia ukuaji wa uchumi wa taifa.

Mkuu wa Idara ya Mawasiliano na Mahusiano kwa Umma wa Benki ya Taifa ya Biashara (NBC), Bw. Godwin Semunyu (kulia), akipimwa nguo na mwanafunzi wa kozi fupi ya Ubunifu, ushonaji na teknolojia ya nguo katika Chuo cha VETA Kihonda, Amina Rashid (kulia). Amina ni miongoni mwa vijana 588 wanaonufaika na mpango wa ufadhili wa mafunzo ya ufundi stadi kwa vijana unaojulikana kama NBC Wajibika Scholarship, unaotekelezwa na VETA kwa ufadhili wa NBC. Tukio hilo lilifanyika leo mkoani Morogoro wakati wa uzinduzi rasmi wa utekelezaji wa mpango huo.



Hafla hiyo ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa VETA akiwemo Mkurugenzi wa VETA Kanda ya Mashariki, Bw. John Mwanja, aliyemwakilisha Mkurugenzi Mkuu wa VETA, Mkuu wa Chuo cha VETA Kihonda, Dkt. Ulimwengu Salumu, walimu, wanafunzi wanufaika pamoja na maofisa wa NBC wakiongozwa na Bw. Semunyu.

Kupitia mpango huo kila mwanafunzi amefunguliwa akaunti ya “NBC Kua Nasi” ili kuwaunganisha na mfumo rasmi wa kifedha, sambamba na kuwapatia fursa za kukuza ujuzi wa kibiashara kupitia majukwaa ya NBC Business Club pindi watakapomaliza mafunzo hayo.



 

Watumiaji wa petroli wamepata afueni mwezi Juni 2026 baada ya bei ya mafuta hayo kushuka ikilinganishwa na mwezi uliopita. Kwa Dar es Salaam, petroli sasa itauzwa kwa bei kikomo ya shilingi 4,086 kwa lita, hatua inayotarajiwa kupunguza gharama kwa watumiaji wa kawaida na baadhi ya shughuli za usafiri.

Kwa upande wa dizeli, watumiaji wanakabiliwa na ongezeko dogo la bei, ambapo kwa Dar es Salaam bei kikomo imefikia Shilingi 4,333 kwa lita. Ongezeko hilo limechangiwa na kupanda kwa gharama za mafuta katika soko la dunia pamoja na kuongezeka kwa gharama za uagizaji wa bidhaa hiyo.

Licha ya changamoto hizo za kimataifa, Serikali imeendelea kuchukua hatua za kulinda uchumi na wananchi kwa kuweka ruzuku ya Shilingi 534.91 kwa kila lita ya dizeli. Hatua hiyo imelenga kupunguza athari za ongezeko la bei kwa sekta muhimu kama usafirishaji, viwanda na huduma za kijamii.

Mabadiliko haya yameathiriwa kwa kiasi kikubwa na vita vinavyoendelea Mashariki ya Kati, vinavyohusisha Marekani, Israeli na Irani. Mgogoro huo umeathiri uzalishaji, uhifadhi na usafirishaji wa mafuta duniani, huku kufungwa kwa Mlango Bahari wa Hormuz kukiongeza gharama za usafirishaji na bima za meli za mafuta.


Na Janeth Raphael - MichuziTv - Bungeni Dodoma


Serikali imesema inaendelea kuchukua hatua mbalimbali za kulinda biashara na mitaji ya vijana kwa kuhakikisha wakandarasi na wazabuni wanalipwa kwa wakati pamoja na kuongeza ushiriki wao katika fursa za zabuni za umma.

Kauli hiyo imetolewa bungeni na Naibu Waziri wa Fedha, Laurent Luswetula, alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Timida Mpoki Fyandomo, ambaye alitaka kufahamu hatua zinazochukuliwa na Serikali kulinda biashara na mitaji ya vijana dhidi ya ucheleweshaji wa malipo ya madeni ya wakandarasi.

Luswetula amesema kupitia Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali wa Muda wa Kati wa mwaka 2026/27 hadi 2027/28, Maafisa Masuuli wa Wizara, Idara Zinazojitegemea, Wakala wa Serikali, Ofisi za Wakuu wa Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa wameelekezwa kuweka kipaumbele kwa wawekezaji wa ndani katika utoaji wa zabuni, masharti ya mikataba na ulipaji wa madai yao.

Amesema Serikali pia imeelekeza kuimarishwa kwa ushirikiano wa ubia (joint venture) katika mikataba inayohusisha kampuni za kigeni ili kuongeza ushiriki wa wazawa, hususan vijana, katika miradi mbalimbali ya maendeleo.

Aidha, Naibu Waziri huyo amesema Serikali imetenga shilingi bilioni 700 katika mwaka wa fedha 2025/26 kwa ajili ya kulipa madeni ya wakandarasi na wazabuni.

Amebainisha kuwa katika kipindi cha Julai 2025 hadi Februari 2026, jumla ya shilingi bilioni 477.6 tayari zimelipwa kwa wakandarasi mbalimbali nchini.

Luswetula amesisitiza kuwa Serikali itaendelea kulipa madeni yaliyosalia kwa lengo la kulinda mitaji ya wakandarasi wa ndani, wakiwemo vijana, na kuwawezesha kuendelea kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo nchini.




Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa amesimama wakati akipokea heshima ya wimbo wa Taifa mara baada ya kuwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Vnukovo, Jijini Moscow kwa ajili ya Ziara ya Kitaifa nchini Urusi tarehe 02 Juni, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Vnukovo, uliopo Jijini Moscow kwa ajili ya Ziara ya Kitaifa, nchini Urusi tarehe 02 Juni, 2026. Ziara hii ina lenga kuimarisha uhusiano wa Kidiplomasia, kisiasa, kiuchumi na kihistoria baina ya Tanzania na Urusi.

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Vnukovo, uliopo Jijini Moscow kwa ajili ya Ziara ya Kitaifa, nchini Urusi tarehe 02 Juni, 2026. Ziara hii ina lenga kuimarisha uhusiano wa Kidiplomasia, kisiasa, kiuchumi na kihistoria baina ya Tanzania na Urusi.


Top News