Ushirikiano kati ya VETA, Enabel na kiwanda cha Kasulu Sugar umeanza kuzaa matunda baada ya vijana 36 waliokuwa wakifanya kazi bila vyeti kutathminiwa na kupatiwa vyeti kupitia mfumo wa urasimishaji wa ujuzi (RPL).

Meneja Rasilimali Watu wa Kasulu Sugar, Samweli George Aoram, amesema hayo wakati Mkurugenzi Mkuu wa VETA, CPA Anthony Kasore, alipotembelea kiwanda hicho Aprili 9 hadi 10, 2026.

Amesema hatua hiyo imechangiwa na ushirikiano thabiti baina ya taasisi hizo, akibainisha kuwa pia wanafunzi 20 kutoka VETA Kasulu wanaendelea na mafunzo kwa vitendo kiwandani hapo huku wakichangia uzalishaji.

Aoram amesema kampuni iko tayari kuendeleza ushirikiano huo ili kupata wataalamu wenye ujuzi unaoendana na mahitaji ya kazi.

Naye Meneja wa Mradi wa Wezesha Binti kutoka taasisi ya Enabel, Christine Karungi, amesema lengo ni kuelewa mahitaji ya waajiri ili kuhakikisha mafunzo yanayotolewa yanatatua changamoto za ajira kwa vijana.

Mkurugenzi Mkuu wa VETA, CPA Anthony Kasore, amesema ushirikiano kati ya taasisi za mafunzo na viwanda ni nguzo muhimu katika kuzalisha wahitimu wenye ujuzi unaokidhi mahitaji halisi ya soko la ajira.

Amesema ziara hiyo imelenga kujionea mahitaji ya ujuzi viwandani na kuimarisha ushirikiano utakaosaidia kuboresha mitaala ya mafunzo ili iendane na mazingira ya kazi.

Amefafanua kuwa kupitia ushirikiano huo, VETA inalenga kuandaa mitaala inayozingatia mahitaji ya waajiri pamoja na kuongeza fursa za mafunzo kwa vitendo kwa wanafunzi.

“Ushirikiano wa karibu na viwanda utatusaidia kuandaa wahitimu watakaoanza kazi moja kwa moja bila kuhitaji mafunzo ya ziada,” amesema.

Aidha, amesema hatua hiyo inawajengea uwezo wakufunzi kwa kuwapatia uzoefu wa teknolojia za kisasa viwandani, hali inayoongeza ufanisi wao wanaporejea kufundisha.












Serikali itahakikisha vipaumbele vya Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Miaka Mitano (FYDP IV) vinaakisi uhalisia wa mchango wa Sekta Binafsi, inayotarajiwa kuchangia takribani 70% ya Pato la Taifa (GDP) ifikapo mwaka 2050.

Hatua hiyo imebainishwa na Naibu Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Mipango, Dr. Blandina Kilama leo Aprili 13, 2026, wakati akifungua Warsha mahususi inayolenga kutoa fursa ya kujadili kwa kina, kukusanya maoni, uzoefu na mapendekezo ya wadau kutoka Sekta ya Umma, na Sekta Binafsi kuhusu maeneo sita (6) ya kipaumbele ya Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Miaka Mitano, sambamba na mwelekeo wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

“majadiliano haya yanalenga kuhakikisha kuwa mchango wa Sekta Binafsi unatambuliwa, unathaminiwa na kuingizwa kikamilifu katika uundaji na utekelezaji wa vipaumbele pamoja na mikakati ya maendeleo, ili kuimarisha ufanisi, kuongeza kasi ya utekelezaji wa FYDP IV, na kufikia matokeo yenye tija na endelevu kwa taifa” Amesema Dkt. Kilama.

Aidha, katika Warsha hiyo, washiriki watajadili mada mahususi zilizomo katika FYDP IV, ikiwemo Kujenga Uwezo wa Watu na Maendeleo ya Jamii, Kutumia Vichocheo vya Maendeleo, Mageuzi ya Sekta muhimu, Uadilifu wa Mazingira na Uhimilivu wa Tabianchi, Uchumi Imara, Jumuishi na Shindani na Kuimarisha Misingi ya Uendelevu wa Taifa.

Dkt. Kilama amesisitiza kuwa, matokeo ya warsha hiyo hayatabaki kuwa nadharia pekee, bali yatatumika katika kuboresha sera, mipango na mikakati ya maendeleo ya taifa.

Na John Mapepele, New York -Marekani  

Waziri wa Afya Mhe. Mohamed Mchengerwa ameongoza timu ya Tanzania katika Mkutano wa 59 wa Kamisheni ya Idadi ya Watu na Maendeleo unaofanyika New York Nchini Marekani.

Mhe. Mchengerwa amesema Mkutano huo ambao umeanza leo Aprili 13,2026 na utaendelea  hadi Aprili 17, 2026 unalenga kuimarisha uhusiano kati ya idadi ya watu, teknolojia, utafiti na maendeleo endelevu, pamoja na kusaidia nchi kupanga sera bora za maendeleo kulingana na takwimu na ubunifu wa kiteknolojia. 

Mhe.Mchengerwa amefafanua kuwa mambo mengine muhimu yatakayojadiliwa wakati wa vikao hivyo ni pamoja na Teknolojia katika afya ya uzazi na afya ya jamii ikiwemo teknolojia mpya za uzazi wa mpango (contraception), Utafiti katika "reproductive health", matumizi ya "telemedicine na digital health platforms" pamoja na upatikanaji wa huduma za afya kwa vijana na wanawake.

Aidha, Mhe. Mchengerwa ambaye pia ameambatana na Naibu Katibu Mkuu anayeshughulikia eneo la Madawa na Vifaa Tiba, Bwana Emmanauel Tayari anayetarajia  kutoa mada  mahususi kwenye mkutano huo kuhusu  Tanzania.

Sanjari na vikao hivyo, Mhe. Mchengerwa anatarajia pia kuwa na vikao kadhaa na wakuu mbalimbali wa mashirika  ya Afya, na mabalozi  wa nchi mbalimbali kuzungumzia  masuala  mbalimbali ya kimkakati katika sekta  ya Afya.

Mkutano huu unahusisha zaidi ya nchi 193 kutoka sehemu mbalimbali duniani pamoja  na mashiriki  yote  makubwa yanayojishuhulisha na  masuala ya afya.








Na Said Mwishehe, Michuzi TV

MWENGE wa Uhuru mwaka 2026 umeweka mawe umekagua  miradi saba katika Wilaya ya Ilala mkoani Dar es Salaam ikiwemo ya afya,elimu, Uwezeshaji wananchi ,barabara na maendeleo ya jamii ambayo imegharimu Sh.bilioni 51.8.

Katika mwenge wa uhuru 2026 kauli mbiu yake inasema “Tanzania ni yetu sote, tushikamane kwa pamoja kuleta maendeleo” ambapo maelfu ya wananchi wa Wilaya ya Ilala wamejitokeza kwa wingi kushuhudia mwenge huo wakati ukitembelea miradi hiyo.

Akizungumza baada ya kutembelea,kukaguwa na kuweka mawe ya msingi katika miradi hiyo Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka 2026 Kitaifa Wazo Mwang’onda amepongeza ujenzi wa miradi hiyo sambamba na kutoa baadhi ya maelekezo kwa viongozi wa Wilaya hiyo ikiwemo kuongeza matanki katika mradi wa kisima cha maji Mchikichini.

Mwenge wa Uhuru ulianza kwa kutembelea mradi mkubwa wa kitega uchumi cha DDC Kariakoo unaojulikana kama DDC Kariakoo One Stop Business Complex wenye thamani ya shilingi bilioni 36.7 ambapo mradi huo unatarajiwa kutoa ajira zaidi ya 4000.

Kwa mujibu wa taarifa ya mradi huo ni wa ubia kati ya Shirika la Maendeleo la Jiji la Dar es Salaam (DDC) na mwekezaji binafsi ambapo ujenzi huo umefikia asilimia 98 ya utekelezaji.

Ujenzi huo unahusisha jengo la ghorofa nane lenye zaidi ya maduka 1,016, ofisi, stoo na maeneo ya huduma mbalimbali ikiwemo benki na burudani.Mradi huo utawezesha  Shirika na Serikali kuongeza mapato ambapo kila mwaka itakuwa inapata  Sh. bilioni 2.500.

Mwenge wa uhuru pia uliweka jiwe la msingi katika mradi wa ujenzi wa barabara ya Lindi yenye urefu wa kilomita 1.015 kwa kiwango cha lami ambayo ni sehemu ya maboresho ya barabara za Ilala CBD wenye thamani ya Sh. bilioni 23.5.

Mradi mwingine ni Kisima cha maji Ilala Mchikichini wenye thamani ya Sh. milioni 164.07 na kwa mujibu wa mradi huo unahusisha uchimbaji wa kisima kirefu cha mita 80, ujenzi wa mnara wa tanki la maji la lita 10,000 na usambazaji wa maji kwenye mtandao wa DAWASA.

Pia Mwenge ulikagua na kuweka jiwe la msingi Kituo cha Afya Mchikichini ambacho ujenzi wake utagharimu Sh.bilioni  7.45.Mradi huo ukikamilika unatarajiwa kuhudumia zaidi ya wananchi 325,000 kutoka kata sita za Ilala na maeneo jirani, hivyo kupunguza msongamano wa wagonjwa katika vituo vingine vya afya.

Mradi mwingine uliotembelewa na Mwenge wa uhuru ni Shule ya Sekondari Kitunda Relini ambapo Mwenge uliweka jiwe la msingi katika ujenzi wa shule mpya ya Sekondari Kitunda Relini iliyojengwa kwa gharama ya zaidi ya shilingi bilioni 4.21.Shule hiyo ya ghorofa itakuwa na madarasa 16, maabara nne za sayansi, maktaba na ofisi za walimu.

Wakati huo huo Mwenge wa Uhuru ulimalizia na mradi wa kituo cha Polisi Bonyokwa chenye thamani ya shilingi milioni 410.









Na, Mwandishi Wetu - Korogwe, Tanga

Mkurugenzi Msaidizi Sehemu ya Afya Moja kutoka Idara ya Menejimenti ya Maafa, Ofisi ya Waziri Mkuu inayoshughulikia masuala ya Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Dkt. Salum Manyatta, amesema kuwa Mpango Mkakati wa Afya Moja umejikita kuhakikisha wananchi wananufaika kuanzia ngazi ya  Kaya hadi Taifa kupitia utekelezaji shirikishi wa sekta mbalimbali nchini ili kuhakikisha malengo yake yanafikiwa na kuwa na tija kwa jamii kwa ujumla.

Dkt. Manyatta ameyasema hayo Aprili 13, 2026 mkoani Tanga wakati wa kikao kazi cha wataalam cha kuandaa Mpango wa Mkoa wa Afya Moja kilichoratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu Sehemu ya Afya Moja kwa kushirikiana na Shirika lisilo la Serikali la CIHEB Tanzania kupitia Mradi wa Usalama wa Afya Duniani.

Amesema kuwa lengo kuu la kikao hicho ni kuwajengea uwezo Watalamu ngazi ya mkoa kuhusu utekelezaji wa Dhana ya Afya Moja na kuwawezesha kutengeneza Mpango wa Utekelezaji wa Afya Moja wa Mkoa ambacho kitafanyika kwa siku tano kuanzia tarehe 13 hadi 17 Aprili 2026 katika Halmashauri ya Mji wa Korongwe, Mkoani Tanga.

Dkt. Manyatta ameeleza kuwa, lengo la dhana ya Afya Moja ni kupanua na kuimarisha ushirikiano baina ya sekta/taaluma mbalimbali katika hatua zote za kuzuia, kujiandaa na kukabiliana na milipuko ya magonjwa na hatari nyingine za afya zinazohitaji ushiriki wa sekta zaidi ya moja na taaluma mbalimbali.

“Ushirikiano huu pamoja na wadau wengine ikiwemo jamii, kimsingi unaongozwa na sekta/wizara za msingi (lead Ministries) ambazo ni Afya ya Binadamu, Wanyama (Mifugo na Wanyama Pori), Mazingira na Kilimo katika ngazi zote,” alifafanua Dkt. Manyatta.

Alifafanua kuwa, uwepo wa Mpango Mkakati ni muhimu kwani unatarajiwa kuweza kujibu na kutatua changamoto zilizopo katika Mkoa wa Tanga, hivyo utumike kama fursa ya kuhakikisha mkoa unakuwa na uelewa wa pamoja wa masuala ya Afya Moja kwa kuunganisha nguvu ya pamoja na kuweza kufanya kazi pamoja kwani hii ndiyo maana halisi ya dhana ya Afya Moja.

Naye Mwakilishi wa Katibu Tawala, ambaye ni Mganga Mkuu wa Mkoa wa Tanga Dkt. Japhet Simeo amepongeza uratibu wa Ofisi ya Waziri Mkuu kwa namna inavyoendelea kutoa elimu ya masuala ya Afya Moja, na kueleza kuwa mkoa wa Tanga utanufaika kwa uwepo wa Mpango Mkakati wa Afya Moja na kusisitiza kuwa Tanga itautekeleza kwa vitendo na kufanya mkoa  huo kuwa wa mfano 

“....Ifike mahali tutoke katika mambo ya concept to Action, yaani kuwa na mipango na mikakati ya namna hii na kuitekeleza na hiyo ndiyo umuhimu wa dhana Afya Moja,” alisisitiza Dkt. Simeo

Kwa upande wake, Msimamizi wa  Afya Moja na Mratibu wa Mradi wa Usalama wa Afya Duniani unaotekelezwa na Shirika lisilo la Serikali la  CIHEB Tanzania Dkt. Irene Massawe amesema kuwa, ushirikiano uliopo utasaidia kufanikisha malengo yaliyopo kwa nguvu ya pamoja na kuhakikisha matarajio ya uwepo wa mpango huo yanafika hadi ngazi za chini.

Aliongezea kuwa, sekta husika zikiungana kwa pamoja katika kutekeleza dhana ya Afya Moja itasaidia kudhibiti vihatarishi vya afya ikiwemo magonjwa ya mlipuko hasa yale yanayoweza kutoka kwa wanyama kwenda kwa binadamu, yakiwemo ya kimeta, kichaa cha mbwa kwani itarahisisha na kuleta ufanisi katika kukabiliana na changamoto hizo.

“Tunaamini kuwepo kwetu ndani ya siku tano hizi Korogwe kutazaa matunda kwa washiriki wote kisha kuyaleta haya katika utekelezaji wa kila siku na kuhakikisha tunaleta matokeo chanya  ya mipango hii,” alisema Dkt. Irene.

AWALI

Afya Moja ni Dhana ya Kimataifa iliyoridhiwa na Shirika la Afya Duniani (WHO), shirika linaloshughulika na Afya ya Wanyama (OIE), Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO), Programu ya Kimataifa ya Mazingira (UNEP) kupitia “Global Health Security Agenda” (GHSA) na wadau wengine wa Afya duniani kote.

 Shirika la Afya Duniani (WHO), Shirika linaloshughulika na Afya ya Wanyama (OIE) na Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO) yamekuwa yakishirikiana duniani kote na kutoa wito kwa wataalamu wa sekta za Afya ya Binadamu, Wanyama na Mazingira kuongeza na kuimarisha ushirikiano na mawasiliano ili kuboresha ufanisi katika kukabiliana na tishio la magonjwa ya kuambukiza yanayoenea kutoka kwa wanyama kwenda kwa binadamu na yanayovuka mipaka; tatizo la usugu wa vimelea vya magonjwa na changamoto zingine zinazokabili afya ya jamii zinazohitaji nguvu ya pamoja. 
















NA VICTOR MASANGU,KIBAHA

Wananchi Kata ya Viziwaziwa wamepongeza kwa dhati juhudi zinazofanywa na Mwenyekiti wa chama cha mapinduzi (CCM) Mwalimu Mwajuma Nyamka kwa kushirikiana na Ofisi ya vizazi na vifo katika suala la kuwapatia vyeti vya kuzaliwa.

Wananchi hao wakimemo wana chama wa CCM katika kata hiyo wameyasema hayo wakati wa mwendelezo wa ziara ya Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Kibaha mjini yenye lengo la kuweza kuwashukuru kwa kuweza kukiamini chama na kuweza kuwachagua viongozi katika ngazi ya udiwani,Ubunge,pamoja na nafasi ya Urais.

Wakizungumza kwa nyakati wamesema kwamba wamefarijika sana kwa zoezi hilo ambalo kwa upande wao litakuwa ni mkombozi mkubwa kutokana na hapo awali walikuwa wanakabiliwa na changamoto hiyo ya kutokuwa na vyeti vya kuzaliwa.

"Tunashukuru sana kwa zoezi hili ambalo limeweza kuwa ni msaada mkubwa sana wa kuweza kupata vyeti vya kuzaliwa kwa bei nafuu na sisi atuna budi kumshukuru Mwenyekiti wa CCM Kibaha mji pamoja na Ofisi ya vizazi na vifo,"wamesema.

Naye Mwenyekiti wa Chama cha mapinduzi (CCM) Wilaya ya Kibaha mjini Mwalimu Mwajuma Nyamka amebainisha ameamua kufanya ziara yake ya kushukuru ambayo inakwenda sambamba na kutoa huduma ya utoaji wa vyeti vya kuzaliwa kwa wananchi.

Nyamka amebainisha kwamba zoezi hilo litawahusisha wananchi wote wenye vifa na kwamba lengo lake kubwa ni kuwasaidia wananchi kuwa na vyeti vyao vya kuzaliwa ambavyo pia vitawasaidia kwa kiasi kikubwa katika mambo yao mbali mbali.

Kwa upande wake Msajili kutoka Ofisi ya vizazi na vifo kutoka Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha John Chuwa amesema kwamba hadi sasa wameshatoa huduma katika kata nne za Mbwawa,Visiga,Misugusugu pamoja na Viziwaziwa.

Ziara ya kushukuru ya Mwenyekiti wa chama cba mapinduzi (CCM) Mwalimu Mwajuma Nyamka pia imewatembelea mabalozi wa mashina pamoja na kufanya mkutano wa hadhara uliowajumuisha wananchi na wanachama wa CCM.




Na Farida Mangube, Morogoro

Chuo Kikuu Mzumbe kimezindua Kituo cha Tafiti na Ubunifu wa Akili Unde (CAIRI), hatua inayokuja wakati ambapo taifa linaongeza jitihada za kutumia teknolojia katika kuboresha elimu, tafiti na kukabiliana na changamoto za maendeleo.

Hafla hiyo imefanyika katika Kampasi Kuu ya Morogoro, ikiongozwa na Naibu Makamu Mkuu wa Chuo anayeshughulikia Taaluma, Utafiti na Ushauri, Prof. Hawa Petro, kwa niaba ya Makamu Mkuu wa Chuo, Prof. William Mwegoha. Hafla hiyo pia imehudhuriwa na wataalamu mbalimbali wa teknolojia, watafiti, washirika wa maendeleo kutoka Ubelgiji pamoja na wanafunzi.

Akizungumza katika hafla hiyo, Prof. Hawa alisema dunia ipo katikati ya mapinduzi makubwa ya kiteknolojia yanayoendeshwa na AI hivyo vyuo vikuu haviwezi kubaki nyuma.

“Kituo hiki kitakuwa daraja kati ya maarifa, ubunifu na mahitaji halisi ya jamii,” alisema Prof. Hawa.

Alisema CAIRI itajikita katika tafiti zenye tija na ubunifu unaotekelezeka kwa ushirikiano kati ya serikali na sekta mbalimbali ili kuhakikisha teknolojia hiyo inaleta matokeo yanayoonekana kwa wananchi.

Kwa upande wake, Mratibu wa mradi huo, Dkt. Bokigwe Isagah, ambaye pia ni mhadhiri wa Chuo Kikuu Mzumbe, alisema lengo la mradi huo ni kufanya tafiti na bunifu zitakazowawezesha wanafunzi wa sayansi kutumia AI katika kutatua changamoto za jamii.

Alisema licha ya serikali kuimarisha matumizi ya teknolojia katika sekta ya elimu, bado kuna changamoto, hivyo chuo kimeona ni muhimu kutumia Akili Mnemba kama suluhisho la kusaidia kuboresha ufundishaji na ujifunzaji pamoja na kutatua changamoto mbalimbali za kielimu katika jamii.

Mwakilishi wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Othman Mohamed, alisema uzinduzi wa kituo hicho ni sehemu ya utekelezaji wa mkakati mpana wa taifa wa kuingia katika uchumi wa kidijitali.

“Akili Mnemba tayari inabadilisha dunia kuanzia elimu, afya, kilimo hadi usalama wa taifa. Tanzania haina budi kuwa sehemu ya mabadiliko hayo,” alisema.

Aliongeza kuwa serikali inaendelea kuandaa mkakati wa kitaifa wa AI, sambamba na kuimarisha matumizi ya teknolojia hiyo katika sekta ya elimu kupitia uboreshaji wa miundombinu ya TEHAMA na kuweka miongozo ya matumizi sahihi ya teknolojia hizo.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Ubunifu, Utafiti na Maendeleo wa Tume ya Taifa ya Mipango, Dkt. Evodius Kanyamyoga Marco, alisema uzinduzi wa CAIRI unaendana moja kwa moja na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, inayolenga kuijenga Tanzania kuwa uchumi unaotegemea maarifa, ubunifu na teknolojia.

Alisema katika kipindi cha awali cha utekelezaji wa dira hiyo, serikali inaweka mkazo katika matumizi ya teknolojia kama kichocheo cha uzalishaji, ajira na ushindani wa kiuchumi.

“Hatuwezi kufikia malengo ya Dira 2050 bila kuwekeza kwa nguvu katika sayansi, teknolojia na ubunifu. Kituo hiki ni hatua ya vitendo kuelekea huko,” alisisitiza.

Mwalimu Debora Maliango kutoka Shule ya Msingi Mzumbe ameishukuru Wizara ya Elimu kupitia Chuo Kikuu Mzumbe kwa kuanzisha mradi huo, akisema umeongeza hamasa ya wanafunzi kujifunza na kupunguza utoro shuleni.

Alisema tangu kuanza kutumika kwa Akili Mnemba katika somo la hisabati shuleni hapo mwaka 2024, imeisaidia kurahisisha ufundishaji kwa walimu na kuboresha ufaulu wa wanafunzi. Aidha, alieleza kuwa endapo utaendelezwa zaidi, mradi huo una uwezo wa kuleta mageuzi makubwa katika mchakato wa ufundishaji na ujifunzaji.

“Hapo awali ilikuwa vigumu kuwavutia watoto darasani, lakini sasa wana hamu ya kujifunza, wanashiriki zaidi, na hata utoro umepungua kwa kiasi kikubwa,” alisema.









Top News