Tume ya Uchunguzi wa Matukio ya Uvunjifu wa Amani yaliyotokea wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025, imesema jumla ya watu 518 walipoteza maisha kutokana na ghasia zilizojitokeza siku ya uchaguzi huo.
Akiwasilisha ripoti ya Tume hiyo leo Ikulu jijini Dar es Salaam leo, Mwenyekiti wake Jaji Mkuu Mstaafu Mohamed Othman Chande amesema vifo hivyo vilitokea katika maeneo mbalimbali nchini, huku Mkoa wa Dar es Salaam ukiongoza kwa idadi kubwa zaidi ya wahanga.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, Dar es Salaam ilirekodi vifo 182, ikifuatiwa na Mwanza (90), Mbeya (80), Arusha (53), na mikoa mingine ikiwa na jumla ya vifo 113.
Jaji Chande amesema kati ya watu 518 waliofariki, wanaume ni 490 sawa na asilimia 94.6, huku wanawake wakiwa 28 (asilimia 5.4). Aidha, alibainisha kuwa sehemu kubwa ya vifo hivyo vilikuwa vya aina isiyo ya kawaida (unnatural deaths).
“Tathmini ya Tume ni kuwa jumla ya vifo vilivyotokana na ghasia za Uchaguzi Mkuu ni 518. Kati ya hivyo, 21 walikuwa watoto,” alisema Jaji Chande.
Kwa mujibu wa takwimu hizo, watoto waliofariki ni pamoja na 15 wenye umri kati ya miaka 15–17, wanne wenye miaka 7–10, na wawili chini ya miaka mitano.
Ripoti hiyo pia imeeleza kuwa vifo 502 (asilimia 96.9) vilikuwa vya raia, huku 16 (asilimia 3.1) wakiwa ni maafisa na askari wa vyombo vya ulinzi na usalama.
Kuhusu mazingira ya vifo hivyo, Tume imesema watu 373 walifikishwa hospitalini wakiwa tayari wamefariki dunia, 121 walifariki wakiwa wanapatiwa matibabu, na miili 24 haikuwa na taarifa kutoka vituo vya huduma za afya.
Aidha, kati ya miili yote 518, miili 480 sawa na asilimia 92.7 ilitambuliwa na kuchukuliwa na ndugu na familia zao.
Ripoti hiyo ni sehemu ya uchunguzi mpana uliofanywa kubaini chanzo na athari za ghasia zilizotokea wakati na baada ya uchaguzi huo.








.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)


.jpeg)


.jpeg)

.jpeg)








.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)


.jpeg)


.jpeg)

.jpeg)












