Awataka waliopewa dhamana ya usimamizi wazingatie misingi ya utawala bora

 
WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba ameziagiza Mamlaka, Taasisi na Wadau wote waliopewa dhamana ya kusimamia utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya Mwaka 2025 wabadilike na wahakikishe wanatekeleza wajibu wao kwa kuzingatia misingi ya utawala bora na utawala wa sheria ili kufikia malengo na shabaha zilizoainishwa katika Sera hiyo.

Amesema taarifa za ukaguzi za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali pamoja na Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma zinaonesha kuwa changamoto katika ununuzi wa umma siyo Sera, Sheria wala Kanuni, bali ni waliopewa dhamana ya kusimamia Sera, Sheria, Kanuni na Taratibu za Ununuzi.

Waziri Mkuu amesema kuwa sehemu kubwa ya shughuli za ununuzi zinaathiriwa zaidi na mitazamo, hulka na tabia za wataalamu na watendaji ikilinganishwa na upungufu wa masuala ya kisera na kisheria, hivyo amewataka  wadau wa Sekta Binafsi waweke mikakati ya kuimarisha mifumo ya ushirikiano na sekta ya umma ili kunufaika kikamilifu na fursa zilizobainishwa katika Sera hiyo.

Ametoa maagizo hayo leo (Jumatano, Aprili 8, 2026) alipozindua Sera ya Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya Mwaka 2025 kwa niaba ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete, jijini Dodoma. “Leo tunaweka alama muhimu katika historia ya usimamizi wa mali na rasilimali za Taifa letu”.

Amesema hatua hiyo ya kisera inalenga kuchochea ukuaji wa shughuli za kiuchumi, kuongeza fursa za ajira na kipato, pamoja na kujenga uchumi jumuishi na shindani unaomilikiwa na Watanzania walio wengi. “Kwa ujumla, fursa hizi zinalenga kuchochea ukuaji wa shughuli za kiuchumi, kuongeza uzalishaji wa bidhaa, Utoaji wa huduma pamoja na kukuza uwiano wa upatikanaji wa bidhaa na huduma”.

“Hii ni kutokana na ukweli kwamba, kwa mara ya kwanza, Tanzania inakuwa na mwongozo mmoja wa kisera unaounganisha na kufungamanisha mtazamo wa kimfumo na hatua zote muhimu katika mnyororo wa ugavi, kuanzia ununuzi, ugomboaji, upokeaji, urejeshaji, uhifadhi, matumizi, usambazaji hadi uondoshaji wa mali za umma”.

Waziri Mkuu amesema Sera hiyo inaweka mkazo katika matumizi ya malighafi na wataalamu wa ndani, kukuza viwanda vya ndani, kuimarisha miundombinu ya kiteknolojia, pamoja na kuzingatia hifadhi ya mazingira na kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi. “Kwa kufanya hivyo, mnyororo wa ugavi umeimarishwa na kuwa chombo cha kimkakati cha kuongeza uzalishaji na ugavi wa bidhaa na huduma pamoja na uendelevu na ushindani wa Taifa katika Masoko ya kikanda na kimataifa”.

Wakati huo huo, Waziri Mkuu amezitaka Wizara, Idara zinazojitegemea, Wakala za Serikali, Taasisi na Mashirika ya Umma, Ofisi za Wakuu wa Mikoa, Mamlaka za Serikali za Mitaa na Wadau wa Sekta Binafsi watekeleze Sera hiyo kwa Weledi, Uwazi na Uwajibikaji.

Amesema kufikiwa kwa malengo na shabaha za Sera hiyo kutategemea zaidi dhamira, fikra, mtazamo, uwazi, ushirikishwaji na uwajibikaji wa wadau wote katika ngazi zote za usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi.

Pia, Waziri Mkuu amezisisitiza Mamlaka zote zinazohusika zihakikishe kuwa utekelezaji wa Sera hii unaimarisha ushiriki wa wazalishaji wa ndani, wafanyabiashara wadogo na wa kati, pamoja na makundi maalumu ya kijamii ili kufikia malengo jumuishi na usawa miongoni mwa washiriki.

Amesema Wizara na Taasisi zote za umma zinapaswa kufanya Mapitio ya Sera, Sheria, Kanuni na Miongozo mbalimbali inayokinzana na misingi ya Sera hii ili kuwa na mazingira rafiki katika usimamizi wa shughuli za Mnyororo wa Ugavi.

Hafla hiyo imehudhuriwa na viongozi mbalimbali akiwemo Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omar, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - Fedha na Mipango, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Dkt. Juma Malik Akil, Mtendaji Mkuu wa Mahakama, Profesa Elisante Ole Gabriel ambaye amemuwakilisha Jaji Mkuu wa Tanzania, Jaji Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti, Mashimba Ndaki aliyemuwakilisha Spika wa Bunge, Wakuu wa Mkoa, Makatibu Tawala wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya, Wakurugenzi wa Halmashauri, Makatibu Tawala wa Wilaya.





 

Na Sixmund Begashe, Dodoma

Wananchi wa Jimbo la Kasulu Vijijini wameendelea kunufaika na uwepo wa mwekezaji katika kitalu cha Makere Forest Reserve kwa kupata mgao wa fedha za maendeleo ya jamii zaidi ya  Shilingi Milioni 12 kila mwaka kinacholipwa na mwekezaji kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo ya vijiji.

Hayo yamesemwa Bungeni Jijini Dodoma na Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji, alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Jimbo hilo Mhe. Edibil Kazala Kinyoma alipotaka kujua "Je, ni kwa kiasi gani wananchi wa Jimbo la Kasulu Vijijini wananufaika na uwepo wa Mwekezaji wa kitalu cha Makere Forest Reserve".

Dkt. Kijaji amesema kuwa kwa kuzingatia vipaumbele vya vijiji husika katika Mwaka wa Fedha 2024/2025 Vijiji vya Kagera Nkanda, Chekenya na Kabulanzwili vililipwa Shilingi 4,356,435.67 kila kimoja. 

"Vilevile, mgao wa fedha zinazotokana na asilimia 25 ya ada ya wanyamapori wanaowindwa katika kitalu husika kwa mujibu wa Kifungu cha 137 cha Sheria ya Fedha ya Mwaka 2025 zinalipwa na Serikali kwa Halmashauri husika".  Alifafanua Dkt. Kijaji

Ameongeza kuwa asilimia 60 ya fedha hizo hutumika kutekeleza miradi ya maendeleo na asilimia 40 shughuli za uhifadhi katika vijiji vinavyozunguka kitalu husika.

 "Sambamba na manufaa yaliyotajwa, katika kipindi cha mwaka 2024/25 na 2025/26 mwekezaji kwa kushirikiana na Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) wamechangia miradi ya jamii yenye thamani ya shilingi 166,475,000". Aliongeza Dkt. Kijaji 

Aidha, Dkt. Kijaji amesema kuwa fedha hizo zimetumika kufadhili kambi ya huduma ya matibabu ya macho katika Halmashauri ya Kasulu, madawati 100 katika Shule za Msingi Chekenya (25), Nyakasanda (25) na Nyantuku (50) na uchimbaji wa visima vya maji sita (6) katika Shule za Msingi Kamganza, Kasasa, Mwitiri, Chekenya na Nyantuki pamoja na Kituo cha Afya cha Kagerankanda.



 


Na Mwandishi wetu -Dodoma

WAZIRI wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda, ametangaza rasmi kufanyika kwa hafla ya nne ya Tuzo ya Taifa ya Mwalimu Nyerere ya Uandishi Bunifu kwa mwaka 2026, akisisitiza kuwa tuzo hizo zimeendelea kuwa chachu muhimu ya kukuza fasihi ya Kiswahili na kuibua vipaji vya waandishi bunifu nchini.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma Aprili 8, 2026, Prof. Mkenda amesema hafla hiyo itafanyika Aprili 13, 2026 katika ukumbi wa Super Dome, Dar es Salaam, ikiwa sehemu ya maadhimisho ya kumbukizi ya kuzaliwa kwa Baba wa Taifa, Julius Nyerere, aliyetoa mchango mkubwa katika kukuza lugha ya Kiswahili na fasihi.

Prof. Mkenda ameongeza kuwa tuzo hizo zimeendelea kuvutia washiriki wengi zaidi kila mwaka kutoka ndani na nje ya nchi. “Kupitia Taasisi ya Elimu Tanzania (TET), inayoratibu tuzo hizo kwa kushirikiana na kamati huru inayoongozwa na Prof. Penina Mlama, mwaka huu washindani walijitokeza kwa wingi katika nyanja nne kuu: riwaya, hadithi za watoto, tamthilia na ushairi,” amesema Waziri Mkenda.

Hafla ya mwaka huu itapambwa na uwepo wa mgeni rasmi, mshairi mashuhuri duniani Abdilatif Abdalla kutoka Ujerumani, ambaye pia aliwahi kufundisha katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kwa zaidi ya miaka 15, jambo linaloipa hafla hiyo uzito wa kipekee kitaifa na kimataifa.

Aidha, kabla ya hafla hiyo kutangazwa washindi, kutakuwa na mjadala maalum utakaowakutanisha waandishi bunifu wa ndani na nje ya nchi, ukiwahusisha wataalamu mashuhuri akiwemo Dkt. Aida Mutenyo kutoka Uganda na Ferdinand Ndahayo kutoka Rwanda.

Kuhusu mafanikio ya tuzo hizo, Prof. Mkenda amesema tangu kuanzishwa kwake, jumla ya Watanzania 27 wamefanikiwa kushinda katika makundi mbalimbali, huku Serikali ikiwekeza takribani shilingi milioni 800 kwa ajili ya uchapishaji wa vitabu vilivyoshinda na kusambazwa katika shule za Tanzania Bara na Zanzibar ili kuhamasisha utamaduni wa kusoma.

“Tuzo hizi pia zimekuwa zikivutia Watanzania waishio nje ya nchi pamoja na washiriki kutoka mataifa mbalimbali, hali inayoonyesha kukua kwa hadhi ya tuzo hizi kimataifa,” amesema Prof. Mkenda, akishukuru Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Samia Suluhu Hassan kwa kuendeleza uwekaji wa mazingira wezeshi katika kukuza sekta ya fasihi na uandishi bunifu.

Waziri Mkenda pia ameipongeza kamati huru ya tuzo chini ya uongozi wa Prof. Penina Mlama kwa kusimamia mchakato wa upatikanaji wa washindi kwa weledi, haki na uwazi. Aidha, amewaalika wananchi kushiriki katika hafla hiyo itakayoanza saa nane mchana, ambapo mbali na kutangazwa kwa washindi, pia kutakuwa na burudani ya kazi za kibunifu pamoja na majadiliano yatakayochochea maendeleo ya fasihi nchini.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Tuzo ya Taifa ya Mwalimu Nyerere ya Uandishi Bunifu 2026, Prof. Penina Mlama, amesema mwitikio wa washiriki umekuwa mkubwa na unaonyesha kukua kwa tasnia ya uandishi bunifu. Washindi watatu bora kwa kila kipengele watapata zawadi ya fedha taslimu pamoja na fursa ya kuchapishiwa kazi zao.


 


Dar es Salaam, Tanzania 

Tunatambua ongezeko kubwa la hivi karibuni la bei za mafuta ambalo limeongezeka kwa asilimia 33. Kama jukwaa linalolenga kusawazisha unafuu wa nauli kwa abiria na mapato endelevu kwa madereva, tunaendelea kushirikiana na mamlaka husika pamoja na wadau wengine kutathmini athari kamili za mabadiliko haya.

Miongoni mwa hatua zinazoweza kuchukuliwa kufuatia mashauriano haya ni;i) kufanya marekebisho ya nauli kulingana na ongezeko la gharama za mafuta; na/auii) kutekeleza mikakati mbadala itakayo punguza athari zinazotarajiwa katika mapato ya madereva.

Tunapenda kuwahakikishia madereva wote kuwa ustawi wao ni kipaumbele kikuu cha jukwaa letu. 

Tunathamini utulivu wao na ushirikiano unaoendelea na abiria wakati tunachukua hatua za haraka kuelekea suluhu zitakazolinda mapato yao na kuhakikisha huduma zinaendelea kutolewa bila usumbufu kwenye jukwaa letu.

Tunaendelea kusisitiza dhamira yetu ya uwazi, usalama na uthabiti wa muda mrefu katika mfumo wa usafiri nchini Tanzania.

Kampuni ya Barrick Mining Corporation imepokea uamuzi wa Mahakama ya Rufaa ya Ontario kutupilia mbali rufaa ya baadhi ya wakazi wa Tanzania wanaodai kuwepo ukiukwaji wa haki za binadamu unaofanywa na askari wa Jeshi la Polisi la Tanzania karibu na mgodi wa dhahabu wa Kampuni ya North Mara.

Uamuzi huu uliunga mkono uamuzi wa awali wa Mahakama ya Juu ya Ontario ambayo iligundua kuwa Ontario sio jukwaa mwafaka la kushughulikia madai haya na kwamba ni lazima yahukumiwe nchini Tanzania.

Kwa mujibu wa taarifa kwa vyombo vya habari iliotolewa nchini Canada imebainisha kuwa Ushahidi uliowasilishwa wakati wa kesi hii ulithibitisha kwamba Jeshi la Polisi la Tanzania linafanya kazi bila ya kutegema Barrick, ambayo inashikilia sera ya kutovumilia ukiukwaji wa haki za binadamu kwa wafanyakazi, wakandarasi au wahusika wengine wanaofanya kazi kwa niaba yake.

Rais na Afisa Mtendaji Mkuu wa Barrick, Mark Hill, alisema: “Barrick inajivunia kazi yetu nchini Tanzania, ambayo tunaifanya kwa ushirikiano wa karibu na ngazi zote za serikali pamoja na jamii zinazotuzunguka.

Kazi yetu kwa pamoja inazalisha ajira, inachochea maendeleo ya kiuchumi na kuboresha maisha ya Watanzania wengi.”

Kuhusu Barrick Mining Corporation

Barrick ni kampuni inayoongoza duniani ya uchimbaji madini, utafii na maendeleo. Ikiwa na mojawapo ya hazina kubwa zaidi za ubora wa dunia na rasilimali za kudumu muda mrefu za dhahabu na shaba katika sekta hii, shughuli na miradi ya Barrick inahusisha nchi 17 na mabara matano. Barrick pia ni mzalishaji mkubwa wa dhahabu nchini Marekani. Tunaunda thamani halisi, ya muda mrefu kwa washikadau wote kupitia uchimbaji madini unaowajibika, ushirikiano thabiti na mbinu yenye nidhamu ya ukuaji. Barrick inashiriki biashara kwenye Soko la Hisa la New York chini ya alama ya ‘B’ na kwenye Soko la Hisa la Toronto chini ya nembo ya ‘ABX’.



VURUGU ZA “KUIBIWA NYETI” ZATINGISHA RUKWA, WAWILI WAFUNGWA MIEZI SITA JELA

Na Mwandishi Wetu, Rukwa

SIKU za hivi karibuni kumeshuhudiwa taharuki iliyopelekea vurugu na kukosekana kwa amani katika baadhi ya maeneo nchini, ikiwemo Mkoa wa Rukwa, kufuatia madai ya kuzushwa kuhusu kuibiwa kwa viungo vya siri.

Kutokana na hali hiyo, Jeshi la Polisi Mkoa wa Rukwa lilifanya msako Aprili 6, 2026 katika Wilaya ya Sumbawanga na kufanikiwa kuwakamata vijana saba waliodai kuwa wameibiwa nyeti zao. Vitendo hivyo vilichochea wananchi kujichukulia sheria mkononi na kuwashambulia watu wasio na hatia.

Akitoa taarifa hiyo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Rukwa alisema kuwa vijana wawili kati ya waliokamatwa, Haruni William Mengo (24), mkazi wa Kalambazite na Isack Simon Kaniki (19), mkazi wa Mshani, wamefikishwa mahakamani na kutiwa hatiani kwa tuhuma hizo.

Mahakama ya Mwanzo Kipeta, Wilaya ya Sumbawanga, chini ya Hakimu Wiligisi Mbunda, Aprili 8, 2026, iliwahukumu wawili hao kutumikia kifungo cha miezi sita jela kila mmoja.

Ilielezwa kuwa Aprili 6, 2026 katika Kijiji cha Mshani, Wilaya ya Sumbawanga, vijana hao walimzushia Issa Athumani Kidungwe (56), mkazi wa Handeni mkoani Tanga, kuwa ameiba nyeti zao, jambo lililosababisha kushambuliwa na wananchi na kujeruhiwa sehemu mbalimbali za mwili.

Wakati huo huo, watuhumiwa wengine watano bado wanashikiliwa na Polisi, ambao ni Geofrey Milumba Deminic (24), Jafari Nebart Shanjila (25), wakazi wa Kijiji cha Kilangawana, Huruma Geofrey Kasonso (18), mkazi wa Kilyamatundu, pamoja na Costantino Octavian Kiatu (28) na Severino Cosmas Ngonyani (22), wakazi wa Sumbawanga. Taratibu za kuwafikisha mahakamani zinaendelea kukamilishwa.

Jeshi la Polisi limeonya wananchi kuacha tabia ya kuzusha taharuki zisizo na ukweli, huku likisisitiza umuhimu wa kufuata sheria kwa kutoruhusu mtu yeyote kujichukulia hatua mkononi.

Aidha, wananchi wametakiwa kutoa taarifa mapema kwa vyombo vya usalama wanapobaini viashiria vya vurugu au uhalifu ili hatua za kisheria zichukuliwe kwa wakati.

Imetolewa na:
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Rukwa




Na Oscar Assenga, TANGA
MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Tanga imefanikiwa kukusanya kiasi cha shilingi bilioni 406.17 katika kipindi cha miezi tisa kuanzia Julai 2025 hadi Machi 2026, ikilinganishwa na lengo la bilioni 296.3 ukiwa ni ufanisi wa asilimia 137.

Akizungumza kuhusu mafanikio hayo leo Meneja wa TRA Mkoa wa Tanga, Casto John, alisema kuwa matokeo hayo makubwa yametokana na mchango na ushirikiano mzuri wa wadau mbalimbali, ikiwemo Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Wakuu wa Wilaya, pamoja na vyombo vingine vya serikali ambavyo vimekuwa mstari wa mbele kuhakikisha ukusanyaji wa kodi unafanyika katika mazingira salama na tulivu.

Aidha, aliwashukuru walipa kodi wote kwa mchango wao mkubwa akisisitiza kuwa mafanikio hayo ni matokeo ya wananchi kujitokeza kwa hiari kulipa kodi zao


Pia alipongeza ushirikiano kutoka kwa vyama vya wafanyabiashara kama JW na TCCIA, pamoja na taasisi za serikali na binafsi ambazo zimekuwa zikifanya kazi kwa pamoja kama timu.

Katika hatua nyingine, Meneja huyo alisisitiza umuhimu wa kipindi cha makadirio ya kodi (Januari hadi Machi) kwa wafanyabiashara kuhakikisha wanajitokeza kwa wingi huku akiwashukuru walipa kodi waliojitokeza kukadiriwa na kulipa kodi zao.

Hata hivyo, aliwataka wale ambao bado hawajafika kujitokeza haraka kwani ofisi za TRA ziko wazi kwa huduma hiyo.

Alionya kuwa kutakuwa na zoezi la kuwafuatilia wadaiwa wa kodi, likiwemo ukaguzi wa barabarani kwa magari na wafanyabiashara wasiolipa kodi, hivyo ni vyema wakazingatia sheria mapema.

Kuhusu matumizi ya mashine za kielektroniki za kutoa risiti (EFD), amesema bado kuna changamoto katika baadhi ya maeneo kutokana na baadhi ya wafanyabiashara kutokutoa hivyo niwatake


Aliwataka wafanyabiashara kuhakikisha wanatoa risiti kwa kila huduma au bidhaa wanayouza, huku akiwahimiza wananchi kudai risiti wanaponunua bidhaa au kupata huduma.

Pia alibainisha kuwa changamoto zozote zinazohusiana na EFD zinapaswa kuripotiwa ili zipatiwe ufumbuzi.

Akizungumzia suala la magendo, alisema Mkoa wa Tanga unapakana na nchi jirani akionya baadhi ya wafanyabiashara wanaotumia njia zisizo rasmi kuingiza bidhaa nchini .huku akiwataka kutumia mipaka rasmi ili kuhakikisha bidhaa zinakaguliwa na taasisi husika kama TBS kwa ajili ya kulinda afya za wananchi.

Alisisitiza kuwa magendo yana madhara makubwa kwa uchumi wa nchi, kwani husababisha kukosekana kwa takwimu sahihi za biashara, kupunguza mapato ya serikali, na kuathiri wafanyabiashara halali pamoja na wananchi kwa ujumla.





RAIS wa Uganda, Mheshimiwa Yoweri Kaguta Museveni, amekutana na kufanya mazungumzo na Rais mstaafu wa Tanzania na Mwakilishi Maalum wa Umoja wa Afrika (AU) kwa Ukanda wa Pembe ya Afrika na Bahari ya Shamu, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, katika Ikulu ndogo ya Nakasero jijini Kampala, Jumanne tarehe 7 Aprili 2027.

Katika mazungumzo yao, viongozi hao wawili walijadili hali ya kisiasa na kiusalama nchini Sudan Kusini, wakisisitiza umuhimu wa mazungumzo ya amani na maridhiano kati ya pande husika ili kurejesha utulivu wa kudumu.

Rais Museveni alimweleza Dkt. Kikwete kuwa Uganda itaendelea kuunga mkono juhudi zote za kuleta amani nchini humo, akibainisha kuwa utulivu wa Sudan Kusini, hasa katika eneo la Equatoria ambako kuna idadi kubwa ya raia wa Uganda, ni muhimu kwa usalama wa kikanda na ustawi wa kiuchumi.

Dkt. Kikwete, mwenye uzoefu mkubwa wa kidiplomasia katika masuala ya amani barani Afrika, hivi karibuni aliteuliwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika kuwa Mwakilishi Maalum kwa Ukanda wa Pembe ya Afrika na Bahari ya Shamu, jukumu linalolenga kuimarisha juhudi za upatanishi, ushirikiano wa kikanda na utatuzi wa migogoro katika eneo hilo lenye changamoto za kiusalama na kisiasa.

Na Mwandishi Wetu SAME

WANANCHI wilayani Same, mkoani Kilimanjaro, wamewaomba viongozi wa wilaya hiyo kuhakikisha Tamasha la Utalii la Same Festival linafanyika kila mwaka ili kuendelea kukuza uchumi wao na kuboresha maisha ya wananchi wa kawaida.

Ombi hilo limetolewa leo na wakinamama lishe wakati wa joggin ya kuhamasisha tamasha hilo linalotarajiwa kufanyika Aprili 10 hadi 12 mwaka huu, ikiwa ni msimu wa tatu tangu kuanzishwa kwake.

Akizungumza katika joggin hiyo, mama lishe katika stendi ya mabasi wilayani Same, Anna Mzava, alisema kuwa tamasha hilo limekuwa na mchango mkubwa katika kuongeza kipato chao kutokana na ongezeko la wateja kutoka maeneo mbalimbali wanaofika kushiriki.

“Tunaiomba serikali kuhakikisha tamasha hili linakuwa endelevu kwani linatusaidia sana sisi wananchi wa chini. Biashara zetu zinachangamka na tunapata kipato kikubwa zaidi. Kwa mfano, siku za kawaida napika mchele kilo tatu lakini wakati wa tamasha napika hadi kilo kumi na zote zinaisha,” alisema Anna.

Kwa upande wake, Jumanne Idd alisema kuwa tamasha hilo limekuwa chachu ya kuitangaza wilaya ya Same kitaifa, hasa vivutio vya utalii pamoja na vyakula vya asili vya kabila la Wapare.

Alisema kuwa kupitia tukio hilo, shughuli za kibiashara huongezeka kwa kiasi kikubwa, hali inayowezesha wananchi wengi kupata kipato na kunufaika kiuchumi.

Akizungumza kwa niaba ya uongozi wa wilaya, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Same, Yusto Mapande, alisema kuwa wamejipanga kuhakikisha tamasha hilo linaendelea kufanyika kila mwaka kwa lengo la kutangaza vivutio vya utalii vilivyopo wilayani humo.

Mapande aliongeza kuwa halmashauri itaendelea kubuni na kuibua vivutio vipya vya utalii ili kuvifanya vijulikane zaidi na hivyo kuinua uchumi wa wananchi.

“Faida kubwa tunayoitarajia ni kiuchumi. Pale watu wengi wanapokusanyika, kunakuwa na uhitaji wa huduma mbalimbali ambazo wananchi wetu wanazitoa na kulipwa, hivyo kuongeza kipato chao,” alisema Mapande.

Tamasha la Same Festival linatarajiwa kuendelea kuwa jukwaa muhimu la kukuza utalii, biashara na utamaduni wa eneo hilo huku likitoa fursa kwa wananchi kujikwamua kiuchumi.





 

Na Sixmund Begashe, Dodoma

Wananchi wa Jimbo la Kasulu Vijijini wameendelea kunufaika na uwepo wa mwekezaji katika kitalu cha Makere Forest Reserve kwa kupata mgao wa fedha za maendeleo ya jamii zaidi ya Shilingi Milioni 12 kila mwaka kinacholipwa na mwekezaji kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo ya vijiji.

Hayo yamesemwa Bungeni Jijini Dodoma na Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji, alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Jimbo hilo Mhe. Edibil Kazala Kinyoma alipotaka kujua "Je, ni kwa kiasi gani wananchi wa Jimbo la Kasulu Vijijini wananufaika na uwepo wa Mwekezaji wa kitalu cha Makere Forest Reserve".

Dkt. Kijaji amesema kuwa kwa kuzingatia vipaumbele vya vijiji husika katika Mwaka wa Fedha 2024/2025 Vijiji vya Kagera Nkanda, Chekenya na Kabulanzwili vililipwa Shilingi 4,356,435.67 kila kimoja.

"Vilevile, mgao wa fedha zinazotokana na asilimia 25 ya ada ya wanyamapori wanaowindwa katika kitalu husika kwa mujibu wa Kifungu cha 137 cha Sheria ya Fedha ya Mwaka 2025 zinalipwa na Serikali kwa Halmashauri husika". Alifafanua Dkt. Kijaji

Ameongeza kuwa asilimia 60 ya fedha hizo hutumika kutekeleza miradi ya maendeleo na asilimia 40 shughuli za uhifadhi katika vijiji vinavyozunguka kitalu husika.

"Sambamba na manufaa yaliyotajwa, katika kipindi cha mwaka 2024/25 na 2025/26 mwekezaji kwa kushirikiana na Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) wamechangia miradi ya jamii yenye thamani ya shilingi 166,475,000". Aliongeza Dkt. Kijaji

Aidha, Dkt. Kijaji amesema kuwa fedha hizo zimetumika kufadhili kambi ya huduma ya matibabu ya macho katika Halmashauri ya Kasulu, madawati 100 katika Shule za Msingi Chekenya (25), Nyakasanda (25) na Nyantuku (50) na uchimbaji wa visima vya maji sita (6) katika Shule za Msingi Kamganza, Kasasa, Mwitiri, Chekenya na Nyantuki pamoja na Kituo cha Afya cha Kagerankanda.








Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Uvuvi Prof. Mohammed Sheikh,akizungumza leo Aprili 8,2026 wakati akizindua mafunzo ya siku tano kwa maafisa wakaguzi wa mazao ya uvuvi 25 yaliyoandaliwa na Wakala ya Elimu na Mafunzo ya Uvuvi (FETA) kwa kushirikiana na Shirika la Kilimo na Chakula Duniani (FAO).

.....

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Uvuvi Prof. Mohammed Sheikh amewataka wakaguzi wa mazao ya uvuvi kufanya kazi zao kwa ubora ili kulisaidia Taifa kuongeza kiwango cha mazao ya uvuvi yanayosafirishwa nje ya nchi.

Prof Sheikh ametoa kauli hiyo 8 April, 2026 wakati akizindua mafunzo ya siku tano kwa maafisa wakaguzi wa mazao ya uvuvi 25 yaliyoandaliwa na Wakala ya Elimu na Mafunzo ya Uvuvi (FETA) kwa kushirikiana na Shirika la Kilimo na Chakula Duniani (FAO).

"Takwimu zinaonesha kwasasa tunasafirisha tani 60,000 pekee za samaki kwenda nje ya nchi hivyo uwepo wa mafunzo haya uwe chachu ya kuongeza ubora utakaosaidia Taifa kuongeza kiasi cha samaki kinachopelekwa nje ya nchi" Amesema Prof. Sheikh

Kwa uoande wake Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Elimu na Mafunzo ya Uvuvi (FETA) Dkt Semvua Mzighani amesema Mafunzo haya yamelenga kuwajengea uwezo maafisa ukaguzi wa mazao ya uvuvi juu ya taratibu za ukaguzi wa mazao ya uvuvi pamoja na viwango vya ubora vya kitaifa,kikanda na kimataifa.

Pia amewasihi washiriki wa mafunzo kuzingatia mafunzo watakayopatiwa na elimu watakayoipata kupitia mafunzo hayo ikawasaidie wananchi katika maeneo yao.

Awali Mratibu wa mafunzo hayo Mkufunzi Anold Mbunda amesema hii ni awamu ya kwanza ya mafunzo ambapo imejumuisha washiriki toka ukanda wa pwani, awamu ya pili ya mafunzo haya itafanyika mkoani Kigoma ambapo itahusisha washiriki kutoka kanda ya ziwa.



Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Uvuvi Prof. Mohammed Sheikh,akizungumza leo Aprili 8,2026 wakati akizindua mafunzo ya siku tano kwa maafisa wakaguzi wa mazao ya uvuvi 25 yaliyoandaliwa na Wakala ya Elimu na Mafunzo ya Uvuvi (FETA) kwa kushirikiana na Shirika la Kilimo na Chakula Duniani (FAO).



Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Elimu na Mafunzo ya Uvuvi (FETA) Dkt Semvua Mzighani,akizungumza wakati wa mafunzo ya siku tano kwa maafisa wakaguzi wa mazao ya uvuvi 25 yaliyoandaliwa na Wakala ya Elimu na Mafunzo ya Uvuvi (FETA) kwa kushirikiana na Shirika la Kilimo na Chakula Duniani (FAO).



Sehemu ya washiriki wakifatilia hotuba ya Mgeni rasmi Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Uvuvi Prof. Mohammed Sheikh (hayupo pichani) ,wakati akizindua mafunzo ya siku tano kwa maafisa wakaguzi wa mazao ya uvuvi 25 yaliyoandaliwa na Wakala ya Elimu na Mafunzo ya Uvuvi (FETA) kwa kushirikiana na Shirika la Kilimo na Chakula Duniani (FAO).



Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Uvuvi Prof. Mohammed Sheikh,akiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kuzindua mafunzo ya siku tano kwa maafisa wakaguzi wa mazao ya uvuvi 25 yaliyoandaliwa na Wakala ya Elimu na Mafunzo ya Uvuvi (FETA) kwa kushirikiana na Shirika la Kilimo na Chakula Duniani (FAO).

  Na Mwandishi Wetu.

MSIMAMIZI wa Bohari ya kuhifadhia Mafuta (DEPOT)ya MOIL ENERGIES Dkt. Sajad Habib Rai ameipongeza Mamlaka ya Mapato Tanzania(TRA) kwa kuanzisha utaratibu wa kufanya kazi kwa Saa 24 katika maeneo ya bohari kwa lengo la kusaidia kuongeza ufanisi katika utoaji wao huduma.

Aidha akizungumzia kuhusu upatikanaji wa mafuta katika Bohari hiyo, Dkt Sajad ambaye pia ni Meneja Mkuu wa Mansoor Industries, amesema wao kama MOIL ENERGIES wana akiba ya kutosha huku wakisubiri Meli zingine ambazo tayari zimetia nanga zishushe nishati hiyo

Akizungumza siku chache mara baada ya Kamishna Mkuu wa TRA Yusuph Juma Mwenda kutembelea 'Depot' hiyo iliyopo eneo la Kigamboni Jijini Dar es Salaam, Sajad ambaye ni Meneja Mkuu wa Kampuni hiyo alisema kupitia utaratibu huo kwao ni fahari kwa kuwa unarahisisha kazi.

Amesema kutokana na kuongezwa huko kwa muda kwa watumishi wa TRA kuwepo katika maeneo ya kazi kama ambavyo Kamishna Mwenda amesema, shughuli zao zinakwenda kuongezeka ufanisi jambo analosema wamelipokea kwa mikono miwili.

"Kwanza nitumie nafasi hii kumpongeza Kamishina Mwenda kwa utendaji wake wa kazi, kwa sasa TRA imekuwa ikitupa ushirikiano mkubwa wafanyabiashara, kila siku tunaona hatua zaidi na zaidi hili kwetu linatusaidia kufanya kazi Kwa ufasaha" amesema Dkt Sajad

Aidha kuhusu utaratibu mpya wa uuzaji mafuta ya Dizel na Petroli uliowekwa hivi karibuni na TRA , amesema wao kama wafanyabiashara hawana shaka nao kwa kuwa umesaidia kuondoa changamoto ya uchepushaji mafuta na kuhakikisha kila mzigo unaotoka kwenye vituo hivyo unakwenda mahala ulipokusudiwa.

Awali akizungumza wakati wa ziara ya baada ya kutembelea Bohari hiyo na zingine za Uhifadhi wa Mafuta, Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Yusuph Mwenda amesema Mamlaka hiyo imejipanga kutoa huduma kwa Saa 24 katika Bohari za mafuta(Depot) huku akisisitiza uwepo wa udhibiti katika udanyanyifu kutoka kwa watoa huduma hiyo.

"Kama ambavyo Serikali imesema kuwa hakuna upungufu wa mafuta, TRA pia tunasisitiza kuna mafuta ya kutosha nchini kwa zaidi tunawaomba watoa kuzingatia taratibu za uuzaji wa mafuta hayo" amesema Mwenda

Aidha amewataka wauzaji wa mafuta hayo kuhakikisha wanashirikiana na Mamlaka hiyo ili kuwezesha huduma hiyo kutolewa kwa Saa 24 ili kurahisisha kazi ya usambazaji wa mafuta hayo.


Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba akizungumza na Balozi wa Qatar nchini, Fahad Rashid Al-Marekhi, Ofisini kwa Waziri Mkuu Mlimwa jijini Dodoma, Aprili 8, 2026. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)


 

Na. Saidina Msangi, WF, Dodoma.

Serikali imesema kuwa kupitia Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) inaendelea kufanya tathmini ya mahitaji ya ujenzi wa Kituo cha Forodha katika Jimbo la Momba, ikiwemo upembuzi yakinifu, upatikanaji na utambuzi wa eneo, gharama za mradi na utayari wa nchi jirani.

Hayo yalisemwa bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Deogratius Luswetula (Mb), alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Momba, Mhe. Condester Michael Sichalwe, aliyetaka kujua wakati ambao Serikali itajenga kituo cha forodha katika Jimbo la Momba mkoa wa Songwe.

Alisema eneo hilo linaangaliwa kwa kuzingatia ongezeko la shughuli za biashara na umuhimu wake katika kuongeza ufanisi wa ukusanyaji wa mapato na udhibiti wa biashara mipakani.

’’Ujenzi wa vituo vya forodha, ikiwemo katika Jimbo la Momba, hufanyika kwa kuzingatia vipaumbele vya Serikali, ukamilifu wa taratibu na kanuni za kiforodha, utayari wa nchi jirani tunazopakana nazo, masuala ya kiusalama, upatikanaji wa rasilimali fedha, pamoja na tathmini ya umuhimu wa eneo husika katika shughuli za biashara za mipakani,’’ alifafanua Mhe. Luswetula.

Aliongeza kuwa ujenzi wa kituo hicho utaanza mara baada ya kukamilika kwa maandalizi yote muhimu, ikiwa ni pamoja na kupatikana kwa fedha za utekelezaji wa mradi katika bajeti ya Serikali na kutangazwa kwenye Gazeti la Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Aidha, Mhe. Luswetula alieleza kuwa TRA inaendelea na maandalizi na itatoa taarifa rasmi pindi ratiba ya utekelezaji wa ujenzi itakapokamilika na kuielekeza TRA kuharakisha tathmini hiyo ambayo iko katika hatua za mwisho.

Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Deogratius Luswetula (Mb), akijibu swali la Mbunge wa Momba Mhe. Condester Michael Sichalwe, Bungeni Jijini Dodoma, aliyetaka kujua wakati ambao Serikali itajenga kituo cha forodha katika Jimbo la Momba mkoani Songwe.(Picha na Kitengo cha Mawasilino Serikalini, Wizara ya Fedha)

Top News