Mke wa Rais wa Singapore, Mheshimiwa Mama Jane Ittogi Shanmugaratnam, ametembelea kituo cha uzalishaji nguo za pamba zinazotengenezwa kwa mikono Msasani jijini Dar es Salaam na kujionea shughuli mbalimbali zinazofanyika katika eneo hilo.

Akiwa katika kituo hicho, Mheshimiwa Mama Jane Ittogi Shanmugaratnam alitembelea maeneo tofauti ya uzalishaji na kushuhudia hatua mbalimbali za uchakataji wa pamba hadi kutengeneza nguo zinazozingatia ubora wa hali ya juu na utunzaji wa mazingira.

Akiwa katika kituo hicho, alielezwa namna wafanyakazi wa kiwanda hicho wanavyotumia ujuzi wa jadi pamoja na teknolojia za kisasa kuzalisha bidhaa za pamba zinazokidhi mahitaji ya masoko ya ndani na kimataifa.

Mhe. Mama Jane alionesha kufurahishwa na ubunifu, ustadi na juhudi zinazofanywa na watumishi wa kiwanda hicho kidogo na wanavyotumia malighafi za ndani na kusisitiza umuhimu wa kuendeleza ushirikiano wa kimataifa unaolenga kukuza biashara, uwekezaji na maendeleo endelevu.

Rais wa Singapore, Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam na mwenza wake wako nchini kwa ziara ya siku tatu ya kitaifa ikilenga kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi, biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na Singapore.








Na Karama Kenyunko Michuzi Tv

RAIS Samia Suluhu Hassan amesema Tanzania ina fursa kubwa za uwekezaji na iko tayari kuwa lango la Singapore kuingia katika masoko ya Afrika Mashariki, Ukanda wa Maziwa Makuu na Bara la Afrika kupitia Soko Huru la Afrika (AfCFTA).

Akizungumza katika Jukwaa la Biashara na Uwekezaji la Tanzania na Singapore, Rais Samia alisema Tanzania ni moja ya nchi zenye uchumi imara na unaokua kwa kasi barani Afrika, huku ikiwa na nafasi ya kimkakati inayounganisha masoko ya Afrika Mashariki, Kati na Kusini mwa Afrika.

Alisema licha ya mahusiano mazuri ya kidiplomasia kati ya Tanzania na Singapore, bado kuna fursa kubwa ambazo hazijatumika kikamilifu katika biashara na uwekezaji.

Kwa mujibu wa Rais Samia, biashara kati ya nchi hizo iliongezeka kutoka dola za Marekani milioni 74 mwaka 2020 hadi dola milioni 299 mwaka 2023 kabla ya kushuka tena hadi dola milioni 74 mwaka 2024.

Alisema tangu mwaka 1997, Singapore imesajili miradi 36 nchini Tanzania yenye thamani ya dola milioni 535 na iliyozalisha ajira 3,328.

Rais Samia alitaja maeneo yenye fursa kubwa za ushirikiano kuwa ni bandari na usafirishaji, kilimo na usindikaji wa mazao, nishati jadidifu, miundombinu janja, utalii, uchumi wa buluu, huduma za kifedha na utatuzi wa migogoro ya kibiashara.

Alisema Tanzania ni lango la biashara kwa nchi sita zisizo na bandari ambazo ni Burundi, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Malawi, Rwanda, Uganda na Zambia, huku Bandari ya Dar es Salaam ikihudumia sehemu kubwa ya biashara hiyo.

Kwa upande wake, Rais wa Singapore, Tharman Shanmugaratnam, alisema Tanzania ni nchi yenye idadi kubwa ya vijana, rasilimali nyingi za asili, fursa zinazoongezeka za uwekezaji na nafasi ya kimkakati inayounganisha masoko ya kikanda na ya kimataifa.

Alisema ushirikiano kati ya Tanzania na Singapore unaweza kuunganisha uzoefu wa Singapore katika usimamizi wa mifumo yenye ufanisi, huduma za thamani ya juu, uchumi wa kidijitali na usimamizi wa minyororo ya ugavi na hivyo kuzalisha ajira, kuongeza ujuzi na kukuza ukuaji jumuishi wa uchumi.

Rais Samia aliwataka wafanyabiashara na taasisi za pande zote mbili kutumia jukwaa hilo kujenga ushirikiano wa kudumu utakaozalisha uwekezaji, biashara na miradi yenye manufaa kwa wananchi wa nchi hizo mbili.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Singapore, Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam mara baada ya kuwasili Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa Ziara ya Kitaifa, tarehe 09 Juni, 2026.
Na Karama Kenyunko Michuzi Tv

TANZANIA na Singapore zimefungua ukurasa mpya wa ushirikiano baada ya kusaini mikataba mitano na hati za makubaliano katika sekta mbalimbali hatua inayolenga kuimarisha biashara, uwekezaji na ushirikiano wa kiuchumi kati ya nchi hizo mbili.

Mikataba iliyosainiwa inahusi kuondoa kodi Mara mbili (Double Taxation) muendelezaji wa ujuzi, biashara za kaboni, mashauriano ya kidiplomasia na uwezeshaji wa biashara.

Mikataba hiyo itapunguza gharama za kufanya biashara, kupunguza vihatarishi vinavyotazamwa na wawekezaji na kuongeza imani kwa wawekezaji wanaotaka kuwekeza katika nchi hizo mbili.

Amesema nchi hizo pia zinaendelea kufanya kazi kuelekea mfumo wa pamoja wa utekelezaji wa biashara ya kaboni chini ya Kifungu cha sita cha Mkataba wa Paris huku zikihamasisha maendeleo endelevu.

Akizungumza katika Jukwaa la Biashara na Uwekezaji la Tanzania na Singapore jijini Dar es Salaam, Rais Tharman amesema dunia inakabiliwa na mazingira mapya ya biashara yenye kutokuwa na uhakika, hivyo kuna umuhimu wa kujenga njia mpya za ushirikiano wa kiuchumi na minyororo imara ya ugavi.

Kwa upande wake, Rais Samia Suluhu Hassan amesema yeye na Rais Tharman walifanya mazungumzo yaliyowezesha kusainiwa kwa makubaliano na hati za ushirikiano kwa manufaa ya nchi hizo mbili.

Amesema hatua hiyo inaonyesha dhamira ya pande zote mbili kuharakisha utekelezaji wa makubaliano yaliyofikiwa na kuinua uhusiano wa Tanzania na Singapore katika viwango vya juu zaidi.

Rais Samia amesema ziara hiyo ya Rais wa Singapore imekuja wakati nchi hizo zikiadhimisha miaka 45 ya uhusiano wa kidiplomasia na kwamba ni mara ya kwanza katika historia Rais wa Singapore kufanya ziara ya kiserikali nchini Tanzania.

Amesema Tanzania na Singapore zinaendelea kufurahia uhusiano mzuri unaojengwa katika misingi ya kuaminiana, ushirikiano na manufaa ya pamoja.

Na hii ni habari ya pili kuhusu fursa za biashara na uwekezaji.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiongoza Ujumbe wa Tanzania kwenye mazungumzo na Ujumbe wa Singapore uliongozwa na Rais wa Nchi hiyo Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam, tarehe 09 Juni, 2026.

Viongozi hao wawili wamefanya mazungumzo rasmi yaliolenga kuimarisha ushirikiano kati ya Tanzania na Singapore katika maeneo mbalimbali hususani biashara, uwekezaji, maendeleo ya rasilimali watu na ujuzi, pamoja na uchumi wa kidijitali.Mazungumzo hayo yalifuatiwa na utiaji saini wa mikataba na Hati za ushirikiano kati ya nchi hizo mbili, na mkutano wa pamoja na waandishi wa habari.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Singapore, Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam kwenye mkutano na Waandishi wa Habari uliofanyika, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 09 Juni, 2026.



Mstahiki Meya wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Alimwoni Chaula, amefanya ziara ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa Barabara ya Kidia, ambayo ni miongoni mwa barabara zinazoboreshwa kwa kiwango cha lami katikati ya Jiji la Dodoma.

Ujenzi wa barabara hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mh. Dk. Samia Suluhu Hassan, ya kutaka halmashauri za majiji kutenga asilimia 10 ya mapato ya ndani kwa ajili ya ujenzi na uboreshaji wa barabara za mitaa.

Akizungumza wakati wa ukaguzi huo, Mstahiki Meya Chaula aliwataka wananchi kushiriki katika kutunza miundombinu hiyo ili iweze kudumu na kuendelea kutoa huduma kwa muda mrefu.

“Wananchi kwa pamoja tunapaswa kushirikiana katika kuzitunza barabara hizi kwa kufuata taratibu zilizowekwa,Wafanyabiashara waepuke kufanya biashara katika maeneo ya barabarani kwani hali hiyo huchangia uharibifu wa miundombinu hiyo” alisema Chaula.

Aliongeza kuwa halmashauri itaendelea kutoa elimu kwa wafanyabiashara kupitia viongozi mbalimbali wa maeneo husika kuhusu athari za kufanya shughuli za biashara kwenye hifadhi ya barabara.

Kwa upande wake, mfanyabiashara wa eneo hilo, Peter Moshi ameishukuru serikali kwa kutekeleza mradi huo akisema kuwa wananchi walikuwa wakisubiri kwa muda mrefu kuona barabara hiyo ikiboreshwa na kukamilika kwake kutarahisisha shughuli za biashara, kuongeza usafiri wa uhakika na kuchochea maendeleo ya kiuchumi kwa wakazi wa eneo hilo na maeneo jirani.

Barabara zinazotekelezwa katika mpango huo zina jumla ya urefu wa kilometa moja kila moja na zinagharimu takribani shilingi bilioni 1.9 kwa ujumla.







Na Janeth Raphael MichuziTv 


Tanzania na Singapore zimekubaliana kuimarisha na kupanua ushirikiano wao katika nyanja za uchumi, biashara na uwekezaji, katika hatua inayolenga kuongeza tija na manufaa kwa wananchi wa mataifa hayo mawili.

Makubaliano hayo yamefikiwa kufuatia mazungumzo rasmi kati ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, na Rais wa Jamhuri ya Singapore, Tharman Shanmugaratnam, ambaye yupo nchini kwa ziara ya kitaifa ya kihistoria.

Akizungumza leo Jumanne, Juni 09, 2026, baada ya kumpokea mgeni huyo Ikulu, Rais Samia amesema mazungumzo yao yamejikita katika namna bora ya kuimarisha ushirikiano uliopo ili ulete matokeo halisi katika maendeleo ya pande zote mbili.

Amebainisha kuwa licha ya kuwepo kwa ukuaji wa mahusiano ya kibiashara, bado kiwango cha biashara kati ya Tanzania na Singapore hakijafikia matarajio ya nchi hizo. Kwa sasa, biashara kati ya mataifa hayo inakadiriwa kufikia takribani dola za Marekani milioni 299, huku Singapore ikiwa tayari imewekeza kupitia miradi 36 nchini Tanzania.

Rais Samia amesema makubaliano mapya yanalenga kuongeza mtiririko wa biashara, kuvutia uwekezaji zaidi, na kufungua fursa mpya katika sekta mbalimbali muhimu za kiuchumi.

Katika upande wa diplomasia, Tanzania imeiomba Singapore kufungua ubalozi wake nchini, hatua inayotarajiwa kuimarisha zaidi mahusiano ya kidiplomasia na kiuchumi kati ya nchi hizo.

Aidha, viongozi hao wamekubaliana kuanzisha mfumo wa mashauriano ya mara kwa mara utakaosaidia kuratibu mipango ya maendeleo na kushughulikia changamoto zinazoweza kujitokeza katika utekelezaji wa miradi ya ushirikiano.

Katika sekta ya kilimo, Tanzania imeonesha dhamira ya kushirikiana na Singapore katika kuimarisha usalama wa chakula, hatua itakayosaidia kuongeza biashara ya mazao ya chakula pamoja na kuhakikisha upatikanaji wa chakula cha kutosha na cha uhakika kwa pande zote mbili.

Rais Samia pia amesisitiza umuhimu wa kuwawezesha vijana, akibainisha kuwa Dira ya Taifa 2050 imeweka msingi mkubwa wa kuwajenga vijana kama nguzo ya maendeleo ya taifa katika miaka ijayo.

Ziara ya Rais Tharman Shanmugaratnam imeelezwa kuandika ukurasa mpya katika historia ya mahusiano ya Tanzania na Singapore, ikiwa ni mara ya kwanza kwa Rais wa Singapore kufanya ziara ya kitaifa nchini Tanzania tangu kuanzishwa kwa uhusiano wa kidiplomasia kati ya mataifa hayo mawili.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Rais wa Jamhuri ya Singapore, Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam mara baada ya kuwasili Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa Ziara ya Kitaifa, tarehe 09 Juni, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiongoza Ujumbe wa Tanzania kwenye mazungumzo na Ujumbe wa Singapore uliongozwa na Rais wa Nchi hiyo Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam, tarehe 09 Juni, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Waandishi wa Habari kuhusu Ziara ya Kikazi ya Rais wa Jamhuri ya Singapore, Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 09 Juni, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Singapore, Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam akizungumza na Waandishi wa Habari kufuatia Ziara yake ya Kitaifa Jijini Dar es Salaam, tarehe 09 Juni, 2026.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na Rais wa Jamhuri ya Singapore, Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam mara baada ya kuwasili Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa Ziara ya Kitaifa, tarehe 09 Juni, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Singapore, Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam, ambaye amewasili nchini kwa ziara ya Kitaifa ya siku 3, kufuatia mwaliko wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na mwenyeji wake mara baada ya kuwasili ikulu.

Mheshimiwa Rais Tharman Shanmugaratnam ameweka historia ya kuwa Rais wa kwanza kutembelea nchini tangu kuanzishwa kwa mahusiano ya kidiplomasia mwaka 1980.







Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kuiimarisha mifumo ya usimamizi wa nyaraka za kieletroniki ili kuhakikisha taarifa muhimu za Taifa zinahifadhiwa kwa usalama, zinapatikana kwa urahisi na zinadumu kwa muda mrefu.

Hayo yamemwa na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abulla katika maadhimisho ya siku ya nyaraka duniani kwa mwaka 2026 yaliyoadhimisha kitaifa katika viwanja vya Makumbusho ya Amani Mnazi mmoja.

Amesema katika kipindi hiki cha maendeleo makubwa ya teknolojia ya habari na mawasiliano usimamizi wa nyaraka unahitaji kwenda sambamba na matumizi ya mifumo ya kisasa ya kidijitali ili kurahisha upatikanaji wa taarifa na kuongeza ufanisi zaidi.

Mhe Hemed amesema kuwa ni matumaini ya Serikali kuwa taasisi zote za umma na binafsi zitaendelea kuzingatia viwango vya kitaalamu katika usimamizi wa nyaraka na kumbukumbu kwa lengo la kuongeza ufanisi wa utoaji huduma kwa wananchi na kulinda historia ya Taifa la Tanzania.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar amesema kuwa Zanzibar imekuwa kitovu muhimu cha elimu, biashara, ustaarabu na utamaduni katika ukanda wa Afrika Mashariki na bahari ya hindi hivyo Serikali itahakikisha kuwa Manuskripti zinaendelea kuhifadhi maarifa muhimu yanayohusu dini, sheria, elimu, tiba , biashara, utawala na maisha ya jamii kwa ujumla.

Aidha amesema kuwa hati za kale ni ushahidi tosha wa mchango mkubwa wa Zanzibar katika maendeleo ya elimu na ustaarabu wa kiislamu sambamba na kuwa chanzo muhimu cha tafiti kwa watafiti , wanahistoria, wanafunzi na taasisi mbali mbali duniani.

Sambamba na hilo Mhe. Hemed amesema ni wajibu wa kila mmoja kuhakikisha kuwa manuskripti na nyaraka adhimu zinalindwa, zinatunzwa na zinaendelezwa kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho na kuahidi kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na taasisi mbali mbali za ndani na nje ya nchi katika kuhifadhi na kuendeleza urithi huu muhimu kwa Taifa.

Hata hivyo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar ametoa wito kwa wananchi kuthamini utamaduni wa kutunza kumbukumbu na nyaraka muhimu katika maisha yao binafsi, taasisi na jamii kwa ujumla kwani Taifa lenye utamaduni wa kuhifadhi kumbukumbu zake hujenga msingi imara wa maendeleo, uwajibikaji na utambulisho wa vizazi vyake.

Nae waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Ikulu Mhe. Dkt. SAADA MKUYA SALUM amesema uwepo wa taasisi ya Nyaraka huisaidia jamii kujua umuhimu wa nyaraka na kumbukumbu katika kuhifadhi historia, kulinda haki za wananchi, kuimarisha uwazi na uwajibikaji pamoja na kuchangia maendeleo endelevu katika jamii.

Amesema nyaraka ni msingi wa kumbukumbu za Taifa zinazohifadhi ushahidi wa shughuli za Serikali na jamii pamoja na kulinda haki za wananchi, kuimarisha utawala bora na kutoa rejea muhimu kwa vizazi vya sasa na vijavyo.

Aidha Dkt. Saada amefahamisha kuwa katika kuadhimisha siku ya nyaraka duniani taasisi ya nyaraka na kumbukumbu Zanzibar imeandaa na kutekeleza shughili mbali mbali ikiwewmo jukwaa la nyaraka, ziara za kijamii, maonesho ya nyaraka za kihistoria sambamba na maonesho maalumu ya maandiko ya kiislamu na hati za kiarabu.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Nyaraka na kumbukumbu Zanzibar ndugu Khatibu Suleiman Khatibu amesema taasisi hio imejipanga kutoa elimu juu ya matumizi mazuri ya nyaraka na kumbukumbu kwa maslahi ya vizazi vya sasa na baadae.

Ndugu Khatibu ametumia nafasi hio kuitaka jamii kuitumia taasisi ya nyaraka katika utunzaji wa nyaraka na kumbukumbu pamoja na kupata elimu juu ya utunzaji wa nyaraka na kujiepusha na migogoro isiokuwa na tija katika jamii

Mapema Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar amekagua mabanda ya maonesho ya vitu vya asili na tamaduni za kizanzibari.









Na Mwandishi Wetu

KATIKA kuelekea kusherehekea siku ya kucheza duniani (International day of play), Shirika lisilo la kiserikali la BRAC Tanzania limewataka wazazi kutenga muda wao mzuri wa kucheza na watoto ili kuwapa ujasiri na kupata uchangamshi wa kimwili na kiakili.

Hayo yamesemwa na mkufunzi wa makuzi na malezi na maendeleo ya awali ya watoto (ECD Trainer) Mbua Dule wakati wa kuadhimisha siku hiyo ya kucheza duniani kwa kutambua umuhimu wa wazazi kushiriki kwenye michezo ya watoto.

Mbua amesema, jamii ya sasa hivi ni tofauti na jamii ya zamani ambapo wazazi wengi kwa sasa hawana muda wa kukaa na mtoto zaidi anaangalia harakati zake za kimaisha na kusahau majukumu yake kama mzazi au mlezi.

Amesema, mzazi anapocheza na mtoto kunakuwa na muunganiko mzuri wa mahusiano ya mzazi na mtoto, na uoga huwa unapungua na hata ikitokea mtoto amefanyiwa ukatili wa kijinsia wa aina yoyote ile basi anakuwa na uwezo wa kuelezea kwa mzazi wake au mlezi.

“wazazi wengi wamekuwa hawana muda wa kukaa na watoto, ukipata muda wa kucheza na mtoto wako basi unakuwa unampa ujasiri wakati wote na hata anapokwua changamoto ya kufanyiwa ukatili wa kijinsia basi anaweza akakufuata na kukuelezea jambo hilo sababu tayari anakuwa ameshajenga ukaribu Zaidi wa mtoto na mzazi,” amesema Dule.

Amesema, kila mwaka tarehe Juni 11, ni Siku ya kucheza duniani na wao kama BRAC wameamua kushiriki kwa vitendo,wakianzia kwenye maeneo ya jamii na kumalizia kwa wafanyakazi sababu hata pindi wanapliwa wanarudi nyumbani wafahamu umuhimu wa kutenga muda wa kucheza na mtoto.

“tumeanza kwenye jamii katika vituo mbalimbali vya malezi na makuzi ya awali kwa watoto lakini kwa siku ya leo tumeamua kuwashirikisha wafanyakazi , tuwaoe elimu juu ya umuhimu wa kutenga muda wa kucheza na mtoto na hata wanapokuwa wanarudi majumbani wawe wakawa mabalozi wa kuwaelimisha jamii umuhimu wa kutenga muda wa kucheza na watoto wao,”amesema Dule

Dule amesema, duniani ya sasa hivi imetawaliwa na utandawazi zipo katuni zinazotoa elimu, watoto wengi wamekuwa wanatumia muda mwingi kwenye simu za wazazi wao jambo ambalo linawanyima fursa ya kupata muda wa kucheza, hivyo basi wazazi au walezi watenge japo muda wa asilimia 20 hadi 30 kwa ajili ya watoto kucheza ili kukuza uchangamfu wa mwili na akili.

Shirika la BRAC limekuwa linatoa elimu ya makuzi na malezi ya awali kwa wanafunzi katika vituo mbalimbali na wamekuwa wanatoa elimu ya malezi kwa wazazi, ulinzia na usalama kwa watoto. Na vituo hivyo vimekuwa vinatoa fursa ya mabinti zaidi ya 300 kupata fursa ya ajira.
Wafanyakazi wa Shirika la Brac Tanzania wakicheza michezo mbalimbali wakati ya maadhimisho ya siku ya kucheza duniani iliyofanyika katika Makao Makuu ya Ofisi hiyo Jijini Dar es Salaam.






Top News