Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe.Prof.Adolf Mkenda amesema Hafla ya Nne ya Tuzo ya Taifa ya Mwalimu Nyerere ya Uandishi Bunifu Inatarajia kufanyika tarehe 13 Aprili 2026 jijini Dar es Salaam katika ukumbi wa Super Dome Masaki. 

Mhe. Adolf Mkenda ameyasema hayo April 8, 2026 jijini Dodoma, Wakati akizungumza na Waandishi wa Habari amesema, hafla hii hufanyika kila mwaka kuadhimisha siku ya kuzaliwa kwa Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere na kutambua mchango wake katika kukuza lugha ya Kiswahili na utamaduni wa Taifa. 

Ameeleza kuwa Mwaka huu, mashindano yamehusisha nyanja nne za fasihi riwaya, hadithi za watoto, tamthiliya na ushairi.

 "Tunaendelea kukuza kiswahili, kuendeleza vipaji vya uandishi bunifu, kulinda historia na utamaduni wa Taifa, pamoja na kuongeza hifadhi ya vitabu katika maktaba ndio malengo ya tuzo hii", amesema Prof. Mkenda.

 Sambamba na hayo Mhe. Adolf Mkenda amesema, Katika hafla hiyo mgeni rasmi anatarajiwa kuwa mshairi maarufu duniani Abdilatif Abdallah, mwenye asili ya Afrika Mashariki, ambaye aliwahi kufundisha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kwa zaidi ya miaka 15. 

Hafla hiyo itatanguliwa na mjadala wa kitaaluma utakaoshirikisha waandishi bunifu wa Tanzania pamoja na wageni mashuhuri kutoka Uganda na Rwanda.




 

VICTOR MASANGU,KIBAHA .

Chama cha mapinduzi (CCM) Wilaya ya Kibaha  mjini imewapongeza kwa dhati wanachama wake na wananchi kwa ujumla kwa kuweza kukipa kura nyingi za kishindo wakati  wa uchaguzi mkuu uliofanyika octoba 29 mwaka 2026.

Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa chama hicho Mwalimu Mwajuma Nyamka wakati wa ziara maalumu ambayo imeanza leo rasmi katika kata ya Mbwawa yenye lengo  kubwa la kuwashukuru wanachama pamoja na wanannchi.

Katika ziara hiyo ambayo imehudhuliwa na viongozi mbali mbali wa chama hicho pamoja na baadhi ya viongozi wa  jumuiya ya Wazazi,pamoja na jumuiya ya umoja wa wanawake wa (UWT) Kibaha mjini wameweza kuwatembelea  na kuzungumza na baadhi ya mabalozi wa matawi Kata ya Mbwawa.

Mwenyekiti Nyamka amesema kwamba pamoja na ziara hiyo kulenga kutoa shukrani pia ameanbatana na baadhi ya wataalamu kutoka Ofisi ya vizazi na vifo Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha (Rita) kwa  lengo la kuwasaidia wananchi wenye changamoto ya ukosefu wa vyeti vya kuzaliwa.

"Mimi kama mwenyekiti wa chama cha mapinduzi (CCM)  Wilaya ya Kibaha mjini pamoja na  viongozi wenzangu tumeanza ziara rasmi ya kuwashukuru wanachama pamoja na wananchi kwa ajili ya kutoa pongezi na shukrani kwa kukipigania chama kushi da  kwa kishindo katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2026,"amesema Mwenyekiti Nyamka.

Nyamka amebainisha kwamba   amefarijika sana na kitendo cha wanachama wa ccm sambamba na wananchi wote kuweza kupambana na kuchagua mafiga matatu kwa kishindo  katika nafasi ya udiwani,ubunge,pamoja na kiti cha Urais.

Kadhalika amewahimiza wanachama kuendelea kushikamana  kwa kishindo kuanzia ngazi za chini lengo ikiwa ni kuweza kukiimarisha chama ikiwa pamoja na kutekeleza ilani kwa vitendo.

Nao baadhi ya viongozi mbali mbali wa mashina wakizungumza kwa nyakati tofauti wamempongeza kwa dhati Mwenyekiti wa CCM Mwalimu Mwajuma Nyamka kwa kuweza kufanya ziara hiyo  na kwenda kuwatembelea na kuwajulia hali zao.

Mmoja wa balozi kutoka Mbwawa shule shina namba  nne Ramadhani Chuma alikishukuru chama chake kwa kuweza kuona umuhimu mkubwa wa kwenda nyumbani kwake kumtembelea kitendo ambacho kimeweza kumfariji sana.

ZIara ya Mwenyekiti wa Chama cha mapinduzi (CCM) Wilaya ya Kibaha mjini Mwalimu Mwajuma Nyamka imeanza leo rasmi katika kata ya Mbwawa ambapo imetembelea baadhi ya viongozi wakiwemo mabalozi pamoja na kufanya mkutano wa hadhara kwa lengo la kuwashukuru wanachama na wananchi.





 

Na Munir Shemweta, WANMM NAIROBI

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeelezea mafanikio yake katika maendeleo ya miji na sekta ya makazi wakati wa Kongamano la Pili la Miji Africa (2nd African Urban Forum) linalofanyika jijini Nairobi, huku ikitoa wito kwa wawekezaji wa ndani na kimataifa kuchangamkia fursa zilizopo nchini humo.

Hayo yameelezwa jijini Nairobi na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo wakati akitoa tamko la Tanzania likielezea jitihada za Serikali katika kuchochea maendeleo endelevu ya miji na makazi, ikiwa ni pamoja na sera, mipango na mikakati inayotekelezwa kuboresha makazi na upangaji wa miji.

Amesema, Tanzania imepiga hatua kubwa katika utekelezaji wa Ajenda 2063 ya Umoja wa Africa, hasa katika maeneo ya miundombinu, upatikanaji wa nishati, utoaji wa huduma za kijamii na kuimarisha ushirikiano wa kikanda.

‘’Juhudi hizo zinaendana na mkakati wa Bara la Africa wa kuimarisha muunganiko, biashara na maendeleo jumuishi’’. amesema

Aidha, Mhe. Dkt Akwilapo alielezea pia mikakati ya serikali ya Tanzania katika kukabiliana na changamoto za ukuaji wa kasi wa miji pamoja na upungufu wa makazi, ambapo kwa sasa makazi yasiyo rasmi yanakadiriwa kufikia asilimia 67.3.

Amesema, katika kukabiliana na hali hiyo, serikali ya Tanzania inaendelea kutekeleza mageuzi ya sera, kuanzisha mifumo bunifu ya fedha, kuboresha umiliki wa ardhi pamoja na kuhamasisha uwekezaji katika makazi nafuu kupitia ushirikiano kati ya sekta ya umma na binafsi.

Aidha, amesema katika kuboresha upatikanaji mikopo ya nyumba, serikali imeanzisha Taasisi ya Tanzania Mortgage Refinance (TMRC) inayosaidia kupunguza gharama za mikopo, kuongeza muda wa marejesho na kutoa fursa kwa wananchi wengi zaidi kupata huduma za kifedha kupitia mikopo midogo midogo.

Waziri huyo wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi amesisitiza kuwa, serikali ya Tanzania itaendelea kutumia rasilimali zake za asili pamoja na kudumisha amani na usalama ili kuharakisha utekelezaji wa Ajenda 2063.

Vilevile, Dkt Akwilapo alitoa wito kwa washirika wa maendeleo na sekta binafsi kushirikiana na serikali katika kuwekeza kwenye sekta ya makazi aliyoieleza kuwa inao mchango mkubwa katika kukuza uchumi na kuboresha maisha ya wananchi.

Kupitia Kongamano hilo, Dkt Akwilapo alieleza salamu za dhati kutoka kwa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliyempongeza Mhe. William Ruto pamoja na wananchi wa Jamhuri ya Kenya kwa kuandaa Kongamano hilo muhimu.

Kongamano la Pili la Miji Africa limezinduliwa rasmi April 9, 2026 na Rais wa Kenya Mhe. William Ruto na linaongozwa na kauli mbiu isemayo “Adequate Housing for All: Advancing Socio-Economic and Environmental Transformation Towards the Realization of Agenda 2063,” ikilenga kuhamasisha mijadala inayotoa fursa kwa washiriki kutoka nchi mbalimbali za Africa kubadilishana uzoefu na suluhisho bunifu katika kukabiliana na changamoto za maendeleo ya miji na makazi.

Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akisoma tamko la Tanzania katika Kongamano la Pili la Miji Africa (2nd African Urban Forum) linalofanyika jijini Nairobi nchini Kenya.



Ujumbe wa Tanzania ukiwa katika Kongamano la Pili la Miji Africa (2nd African Urban Forum) linalofanyika jijini Nairobi nchini Kenya.



Sehemu ya washiriki wa Kongamano la Pili la Miji Africa (2nd African Urban Forum) wakiwa katika kongamano hilo linalofanyika jijini Nairobi nchini Kenya. ( PICHA ZOTE NA WIZARA YA ARDHI)

 

Mbunge wa Jimbo la Kisarawe, Dkt. Selemani Jafo,akichangia makadirio ya mapato na matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zake kwa mwaka wa fedha 2026/27  leo Aprili 9,2026 bungeni jijini Dodoma.

...

Mbunge wa Kisarawe, Dkt. Selemani Jafo, amedhamiria kuwasilisha hoja binafsi bungeni itakayolenga kuishauri Serikali kuanzisha mpango maalum wa mikataba ya ajira za muda mfupi kwa vijana ili kupunguza changamoto ya ukosefu wa ajira nchini.

Akichangia makadirio ya mapato na matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zake kwa mwaka wa fedha 2026/27 bungeni, Jafo alisema mpango huo unaweza kuwa na mfumo wa Ajira za muda (part time employment) utakaodumu kwa kipindi cha miaka mitatu mitatu hadi ifikapo mwaka 2050  ambapo vijana watapata ajira za mikataba na kujipatia uzoefu wa kazi.

Alimpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, kwa juhudi kubwa za kuongeza fursa za ajira kwa vijana tangu aingie madarakani, akisema serikali imefanya kazi kubwa katika kuwawezesha wananchi, lakini bado kuna haja ya kuja na mikakati mipya ya kukabiliana na wimbi la vijana wasio na ajira.

Jafo alibainisha kuwa changamoto ya ajira bado ni kubwa, huku akitoa mfano wa vijana wengi waliopo kwenye shughuli zisizo rasmi kama bodaboda, baadhi yao wakiwa na elimu ya juu ikiwemo stashahada,  shahada na kuendelea. Alipendekeza mpango maalum utakaolenga wahitimu hao ili kuwapa nafasi ya kupata ajira za muda na mikataba ya miaka mitatu.

Kwa mujibu wa mapendekezo yake, kila mwaka vijana 50,000 wanaweza kuingizwa kwenye mpango huo, ambapo asilimia 20 wawe wahitimu wa stashahada na asilimia 80 wawe wahitimu wa shahada na kuendelea. Aidha, alipendekeza malipo ya kujikimu ya Shilingi 500,000 kwa wenye stashahada na Shilingi 700,000 kwa wahitimu wa shahada.

Alisema gharama ya utekelezaji wa mpango huo inakadiriwa kufikia Shilingi bilioni 396, huku akisisitiza kuwa mpango huo utasaidia kukuza ujuzi wa vijana, kuongeza uzoefu wa kazi na kupunguza tatizo la ajira nchini.

Pia alipendekeza asilimia 10 zitoke katika mapato ya ndani ya kila Halmashauri, 10 ya gawio la Serikali kutoka kwenye mashirika ya umma, na fedha zingine zitokane na kubana maeneo mengine ya matumizi ya kawaida ya serikali(Recurrent Expenditure) ili zitumike kufadhili mpango huo. Aidha, alishauri mpango huo usimamie kupitia serikali za mitaa na Taasisi za Umma ili kurahisisha upatikanaji wa ajira katika halmashauri mbalimbali na Taasisi hizo za Umma.

Jafo alisisitiza kuwa mpango huo, kama utapitishwa, utaisaidia Serikali kuongeza wigo wa ajira na kuwawezesha vijana wengi zaidi kunufaika na fursa za kiuchumi nchini.

Kampuni ya Tanzania Breweries Limited (TBL) imetoa wito wa kuwepo kwa hatua za pamoja na endelevu ili kukabiliana na tatizo la pombe haramu nchini, ikionya kuwa hali hii inaendelea kuhatarisha afya ya wananchi, uchumi wa taifa, pamoja na mustakabali wa biashara halali.

Kampuni hiyo imepongeza juhudi zinazoendelea za serikali katika kupambana na biashara haramu, ikibainisha kuwa hatua za hivi karibuni za kukamata na kuondoa bidhaa bandia sokoni zinaonesha dhamira ya kulinda watumiaji na kuhakikisha ushindani wa haki katika soko.

Pombe haramu imeendelea kusambaa kwa kiwango kikubwa nchini Tanzania, ikiwa sehemu muhimu ya matumizi ya pombe na kuwaweka watumiaji wengi katika hatari ya kutumia bidhaa zisizo salama na zisizodhibitiwa. Hali hii imeongeza shinikizo kwa mifumo ya afya, jamii, pamoja na uchumi rasmi.

Kwa upande wa afya, pombe haramu inaleta hatari kubwa. Mara nyingi hutengenezwa bila kufuata viwango vinavyotakiwa, jambo linaloweza kusababisha madhara makubwa kama uharibifu wa viungo vya mwili, kupoteza uwezo wa kuona, na hata vifo.

 Katika jamii nyingi, athari hizi zinaonekana wazi, huku watu wengi wakifahamu mtu aliyepata madhara kutokana na matumizi ya pombe haramu.

Kiuchumi, athari zake ni kubwa. Inakadiriwa kuwa Tanzania inapoteza zaidi ya shilingi trilioni 1 kila mwaka kutokana na mapato yasiyokusanywa yanayohusiana na pombe haramu. 

Haya ni mapato ambayo yangeweza kusaidia kuboresha huduma za afya, kuimarisha elimu, na kuwekeza katika miundombinu kwa manufaa ya wananchi.
Wakati huo huo, biashara haramu inaathiri ushindani wa haki sokoni. 

Wazalishaji wanaofuata sheria na kuchangia uchumi hukutana na ushindani kutoka kwa wafanyabiashara haramu wanaokwepa viwango na kuuza bidhaa kwa bei ya chini. Hali hii inapunguza uwekezaji na kuathiri ajira katika mlolongo mzima wa thamani, kuanzia kwa wakulima, wazalishaji hadi wasambazaji na wauzaji.

Mkurugenzi Mtendaji wa Tanzania Breweries Limited, Michelle Kilpin, amesema kuwa kukabiliana na pombe haramu kunahitaji ushirikiano wa karibu na hatua endelevu.

 Ameeleza kuwa utekelezaji madhubuti wa sheria unapaswa kuambatana na mifumo thabiti ya udhibiti, sera za kodi zinazotabirika, pamoja na kuongeza uelewa kwa watumiaji na wauzaji.

Ameongeza kuwa kupambana na pombe haramu ni jukumu la pamoja kati ya serikali, sekta binafsi na jamii, ambapo kila mmoja ana nafasi ya kupunguza upatikanaji wa bidhaa zisizo salama na kuhamasisha matumizi ya kuwajibika.

Ingawa hatua za utekelezaji wa sheria zinaonesha maendeleo, ukubwa wa tatizo hili unahitaji suluhisho la muda mrefu linalotegemea ushirikiano endelevu na juhudi za pamoja. Upatikanaji rahisi na bei nafuu vinaendelea kuchochea matumizi ya pombe haramu, hasa kwa makundi ya kipato cha chini.

Kwa Tanzania Breweries Limited, msisitizo unaendelea kuwa katika uzalishaji wa bidhaa bora zinazokidhi viwango na kusaidia juhudi za kulinda usalama wa watumiaji pamoja na kuongeza uelewa wa madhara ya pombe haramu.

Kadri Tanzania inavyoendelea kukabiliana na biashara haramu, kulinda watumiaji, kuhifadhi afya ya jamii, na kuhakikisha ushindani wa haki vitabaki kuwa nguzo muhimu katika kujenga soko la pombe lililo salama na endelevu.


 

 Na Leandra Gabriel, Michuzi TV

MSIMU wa mbio za Mac D Promotions ‘ Mac D Marathon’ kwa mwaka 2026 unatarajiwa kufanyika Julai 4 mwaka huu katika viwanja vya Chuo cha Taifa cha Ulinzi (NDC,)  Kwa kauli mbiu ya ‘Go Green With Gas’ yenye kulenga kuhamasisha matumizi ya nishati safi na kutunza misitu.

Akizungumza katika uzinduzi wa mbio hizo uliofanyika katika Hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam Mkurugenzi wa Mipango na Biashara wa Mac D Promotions Denzel Rweyunga amesema kuwa mbio hizo ambazo usajili wake umeanza rasmi leo zinatarajiwa kushirikisha wakimbiaji wa Kilomita 5, 10 na 21 pamoja na mbio za watoto za Kilomita 2.

Amesema kuwa licha ya kuhamasisha utunzaji wa afya kwa kukimbia mbio hizo pia zimelenga kuunga mkono juhudi za Serikali katika kutunza mazingira kwa kuhamasisha matumizi ya nishati safi.

“Tunategemea kuwa na washiriki 3500 katika mbio hizi na maandalizi yameanza mapema ili kuzipa hadhi na viwango vya juu, na tayari usajili umefunguliwa kupitia www.macdmarathon.com na baada ya kujisajili na kufanya malipo kupitia simu au benki washiriki wataweza kupata vifaa zikiwemo tisheti katika vituo mbalimbali vilivyoainishwa.” Amesema.

Akifafanua kuhusu huduma muhimu katika mbio hizo amesema; wamejipanga kwa kuwa na huduma ya kwanza, vituo vya maji safi na salama ya kunywa ya Kilimanjaro, matunda pamoja na ulinzi na washiriki wote watakaofanikiwa kumaliza mbio hizo  watapatiwa medali.

“Mac D Marathon 2026 itarushwa mbashara siku hiyo kupitia vituo vya ITV pamoja na East Africa Televison na baada ya mbio kutakuwa na burudani katika FM Academia chini ya Patcho Mwamba, michezo ya watoto, chakula na vinywaji pamoja na mpira wa miguu kati ya IPP na Mac D promotions.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chama cha Riadha Mkoa wa Dar es Salaam Amani Ngoka amesema kupitia mbio hizo ambazo zimelenga kuhamasisha matumizi ya nishati safi, shirikisho litatumia fursa hiyo kusaka vipaji na wawakilishi wa kimataifa katika riadha.

Aidha amewasisitiza wazazi kushiriki mbio hizo na watoto ambao watakimbia Kilomita 2 ili waweze kutambua na kuendeleza vipaji vyao na kuwataka Mac D promotions kufanya mbio hizo kuwa za kimataifa kwa mwaka ujao.

Kwa taarifa zaidi za ushiriki wa mbio hizo pamoja na udhamini Mac D Promotions itapokea kupitia tovuti pamoja na mawasiliano ya simu 0791799848/0702562009 pamoja na barua pepe macdmarathon@gmail.com.

Mbio za Mac D kwa mwaka 2026 zimedhaminiwa na Shirika la Nyumba la Taifa ( NHC ) , Kilimanjaro Natural Mineral Water, Azania Bank, ITV, Eb Maritime Group, Mart Group Ltd kupitia vinywaji vyake pendwa Tanzanite RoyalGin na Tanzanite Crafted For Royalt, Kaluba, Radio One, EATV, Montage na Ayo Tv.

Mkurugenzi wa Mipango na Biashara wa Mac D Promotions Denzel Rweyunga akizungumza wakati wa uzinduzi wa Mac D Marathon mwaka 2026 na kusema kuwa mbio hizo ambazo usajili wake umeanza rasmi leo zinatarajiwa kushirikisha wakimbiaji wa Kilomita 5, 10 na 21 pamoja na mbio za watoto za Kilomita 2. Leo jijini Dar es Salaam.

Mwenyekiti wa Chama cha Riadha Mkoa wa Dar es Salaam Amani Ngoka akizungumza wakati wa hafla hiyo na kueleza kuwa kupitia mbio hizo ambazo zimelenga kuhamasisha matumizi ya nishati safi, shirikisho litatumia fursa hiyo kusaka vipaji na wawakilishi wa kimataifa katika riadha. Leo jijini Dar es Salaam.


NA EMMANUEL MBATILO, MICHUZI TV

Serikali imeeleza dhamira yake ya kuendelea kuimarisha sekta ya fedha nchini ili iwe chachu ya maendeleo ya haraka ya kiuchumi, huku ikisisitiza upatikanaji wa huduma za kifedha kwa wananchi wote kwa urahisi na gharama nafuu.

Kauli hiyo ilitolewa leo Aprili 9, 2026 jijini Dar es Salaam wakati wa ufunguzi wa jukwaa la wadau wa sekta ya fedha la mwaka 2026, lenye kauli mbiu isemayo “Sekta ya fedha bunifu na yenye uwajibikaji kwa maendeleo endelevu na jumuishi ya jamii na uchumi.”

Akizungumza katika hafla hiyo, Waziri wa Fedha, Khamis Mussa Omari, aliwataka wadau wa sekta hiyo kutumia jukwaa hilo kutoa mapendekezo yatakayosaidia kuboresha sera, sheria na mifumo ya kifedha, ili kufikia lengo la kuwa na uchumi imara unaotegemea sekta ya fedha ifikapo mwaka 2050.

“Sekta ya fedha ni mhimili muhimu wa maendeleo ya taifa. Tunahitaji kuhakikisha huduma za kifedha zinawafikia wananchi wote kwa urahisi na kwa gharama nafuu,” alisema Waziri Omari.

Ameeleza kuwa jukwaa hilo lina lengo la kuwakutanisha wadau mbalimbali ili kujadili utekelezaji wa Mpango Mkuu wa Maendeleo ya Sekta ya Fedha wa miaka kumi (2021–2029), huku akibainisha kuwa sekta hiyo ina mchango mkubwa katika kukuza uchumi na kuongeza upatikanaji wa huduma za kifedha kwa wananchi.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dkt. Natu Mwamba, amesema kuwa katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, kumekuwa na mafanikio makubwa katika sekta hiyo, ikiwemo kuongezeka kwa upatikanaji wa huduma za fedha, ongezeko la matawi na mawakala wa benki pamoja na ukuaji wa huduma za fedha kidijitali.

Amebainisha kuwa asilimia 76 ya Watanzania sasa wanapata huduma rasmi za kifedha, hatua inayochangiwa kwa kiasi kikubwa na matumizi ya simu za mkononi na huduma za fedha mtandao.

Naye Naibu Waziri wa Fedha, Mhandisi Mshamu Munde, amesisitiza umuhimu wa kudhibiti hatari za kifedha ikiwemo biashara haramu na matumizi mabaya ya mifumo ya fedha, huku akihimiza usimamizi madhubuti wa teknolojia mpya za kifedha.

Washiriki wa jukwaa hilo walipata fursa ya kujadili changamoto na fursa zilizopo katika sekta ya fedha, hususan katika maeneo ya ubunifu wa teknolojia, ujumuishwaji wa kifedha na uwekezaji.

Jukwaa hilo linatarajiwa kutoa maazimio yatakayosaidia kuimarisha sekta ya fedha na kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi nchini.

Wadau waliohudhuria ni pamoja na wawakilishi wa mabenki, taasisi za bima, vyama vya ushirika pamoja na sekta binafsi.






 



Na Oscar Assenga, TANGA

Chama cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Tanga kimetoa maelekezo kwa Halmashauri ya Jiji la Tanga kuhakikisha maeneo ya kukusanyia taka katika soko la Mgandini yanaboreshwa kwa kujazwa kifusi ikiwemo kurekebisha barabara za ndani ili kuimarisha usafi.

Agizo hilo lilitolewa na Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Tanga Rajab Abdurhaman wakati wa ziara yake ambapo alisisitiza umuhimu wa kuhakikisha maji ya mvua yanaelekezwa ipasavyo kwenye mifereji ili kuepusha mafuriko na uharibifu wa miundombinu.

Ziara hiyo ilikuwa ni kufuatilia utekelezaji wa maagizo aliyoyatoa awali kuhusu kuboresha usafi wa soko hilo ambapo viongozi wa Jiji hilo walianza kuyafanyia kazi ikiwemo kuondosha uchafuzi uliokuwepo awali.

Awali, wakati wa ziara yake ya kukagua hali ya usafi, Mwenyekiti huyo hakuridhishwa na mazingira ya soko hilo na kutoa muda wa mwezi mmoja kwa uongozi wa Jiji kuhakikisha hali ya usafi inaboreshwa.

Akizungumza baada ya kufanya ziara ya ufuatiliaji, Rajab aliwapongeza Mstahiki Meya pamoja na viongozi wa Jiji kwa kuchukua hatua na kuanza kutekeleza maelekezo hayo ya CCM.

“Hatuhitaji viongozi wa kulalamika, tunahitaji viongozi wanaochukua hatua kutatua changamoto za wananchi. Mlichokifanya ni kutimiza wajibu wenu,” alisema.

Alisema kuwa hali ya uchafu iliyokuwepo awali haikuwafurahisha viongozi wala wafanyabiashara, hivyo hatua zilizochukuliwa zinaonesha uwajibikaji wa uongozi.

Hata hivyo Mwenyekiti Rajab alisisitiza kuwa atarejea kukagua maendeleo hayo baada ya wiki mbili na kuonya kuwa hataki kusikia visingizio badala ya utekelezaji.

“Ndani ya mwezi mmoja kuanzia Aprili 9 hadi Mei 9, tunatarajia kuona kazi imeanza. Hatutaki hadithi, tunataka vitendo,” alisisitiza.

Aidha, alieleza kuwa Jiji la Tanga ni taswira ya mkoa huo, hivyo linapaswa kuwa safi na lenye mpangilio mzuri.

Alikumbusha kuwa zamani Tanga ilikuwa mji unaojulikana kwa usafi na ustaarabu, hivyo ipo haja ya kurejesha hali hiyo.

Kuhusu huduma za vyoo katika soko hilo, Mwenyekiti alieleza kutoridhishwa na hali iliyopo, akibainisha kuwa choo kilichopo hakitoshelezi mahitaji kutokana na idadi kubwa ya watumiaji.

Alisema kuwa hali hiyo inasababisha baadhi ya watu kulazimika kujisaidia katika maeneo yasiyofaa, jambo linalohatarisha afya za wananchi na wafanyabiashara.

Alisisitiza umuhimu wa Jiji kutafuta suluhisho la kudumu, ikiwemo kuboresha mfumo wa maji taka ili kuendana na ongezeko la watumiaji.

Hata hivyo, aliwapongeza viongozi kwa kuanza mpango wa kujenga choo kipya chenye matundu 12 kitakachosaidia kupunguza changamoto hiyo, hasa katika kipindi hiki ambacho soko linatarajiwa kujengwa upya.

Pia alizungumzia changamoto ya msongamano wa magari yanayoleta bidhaa sokoni hapo, akielekeza kuwepo kwa utaratibu maalum wa magari kuingia na kushusha mizigo kwa mpangilio ili kupunguza msongamano na kuboresha usafi.

Alipendekeza magari yapaki katika maeneo maalum yaliyo nje ya soko, kisha yaingie kwa zamu kushusha bidhaa.

Katika hatua nyengine alisisitiza umuhimu wa kujenga mifereji ya maji ili kuzuia maji ya mvua kutuama au kuingia sokoni, hali inayochangia uchafu na uharibifu wa mazingira.

Alimalizia kwa kuwataka viongozi wa Jiji kuwa karibu na wananchi na kushughulikia changamoto zao kwa vitendo, akibainisha kuwa wananchi hao ndio chanzo cha mapato ya Jiji kupitia kodi.

Kwa upande wake, Naibu Meya Khalid Rashid alisema kuwa Jiji lina mpango wa kuboresha miundombinu ya ndani ya soko, ikiwemo njia za kupita ili kuondoa changamoto ya matope wakati wa mvua. Alibainisha kuwa kazi hiyo inatarajiwa kuanza ndani ya wiki moja.

Mwisho.

MAMLAKA ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA) imewatangazia waingizaji wa mizigo mikubwa ya forodha ya bidhaa za Dawa, Vifaa Tiba na Vitendanishi nchini, kuwa mifumo ya TANCIS-TRA na RIMS-TMDA imeunganishwa ili kuongeza ufanisi katika kuingiza na kutoa shehena za bidhaa hizo nchini kwa njia ya kielektroniki.  

Kwa mujibu wa taarifa kwa Umma iliyotolewa na Mkurugenzi Mkuu wa TMDA, Dk. Adam Fimbo ameeleza kuwa, Lengo kuu la muunganiko huo ni kurahisisha michakato ya uombaji vibali kuwa na sehemu moja ya kuingiza taarifa, pamoja na kuboresha ufuatiliaji na shughuli za udhibiti wa maombi ya kuingiza na kutoa bidhaa nchini.

"Mnajulishwa rasmi kuwa kuanzia tarehe 1 Mei, 2026 maombi yote yaliyokuwa yanapitia TMDA-RIMS na TRA-Forodha kwa ajili ya kutolea taarifa (declaration) yatafanyika moja kwa moja katika mfumo wa TANCIS.  

Ili kuepusha Hoja zisizo za lazima na kurahisisha huduma za upatikanaji wa vibali, mnakumbushwa kuzingatia; Usahihi wa taarifa za bidhaa zinazosimamiwa na TMDA (ikijuimuisha namba za usajili za bidhaa na majengo); na Wadau wote watatakiwa kushirikiana na Wakala wa Forodha kwa ukaribu ili kuthibitisha usahihi wa taarifa za kitaalam na nyaraka hitajika." Imeeleza taarifa hiyo kwa Umma.

Aidha, TMDA imewataka kuzingatia kuwa, tangazo hilo  linawahusu waingizaji wa mizigo mikubwa ya forodha, na si waingizaji kwa matumizi binafsi (personal use).

Na Mwandishi wetu, Dodoma

 Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA) imesema ujenzi wa moduli ya kupokea na kushughulikia malalamiko na rufaa katika mfumo wa NeST utachangia kuongeza uwajibikaji, uwazi na ufanisi kwenye mnyororo wa ugavi.

Katibu Mtendaji wa PPAA, Bw. James Sando amebainisha hayo wakati wa uzinduzi rasmi wa Sera Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya Mwaka 2025 na kuongeza kuwa Moduli hiyo imewaunganisha wazabuni wote na Taasisi nunuzi nchini ili kuongeza uwajibikaji katika utatuzi wa migogoro inayotokana na michakato ya ununuzi wa umma. 

“PPAA ni moja kati ya taasisi zinazosimamia ununuzi wa umma nchini, matumizi ya moduli hiyo katika mnyororo wa ugavi yatachangia kutoa maamuzi kwa haki na wakati na kuwezesha miradi ya Serikali kutekelezwa kwa wakati uliokusudiwa,” amesema Bw. Sando.

Pamoja na mambo mengine, Bw. Sando amebainisha kuwa matumizi ya Moduli ya kupokea na kushughulikia malalamiko na rufaa katika ununuzi wa umma yatasaidia kuongeza uwazi, kupunguza gharama, kuokoa muda, utunzaji wa nyaraka na hivyo kuongeza ufanisi katika hukumu zinazotolewa kutokana na michakato mbalimbali ya zabuni za umma.

Bw. Sando ameongeza kuwa, PPAA imefanikiwa kushiriki katika utungwaji wa Sera ya Taifa ya Mnyororo wa Ugavi, Sheria ya Ununuzi wa Umma, Kanunuzi za Ununuzi wa Umma na Kanuni za Rufaa za Ununuzi wa Umma ambapo yote ni michango wa Mamlaka ya Rufani katika mnyororo wa ugavi.

Kadhalika, Mamlaka ya Rufani inatarajia kuboresha kipengele cha makundi maalum na vijana ambapo inategemea kuboresha gharama au tozo za kesi kwa makundi maalum pamoja na kuelekeza nguvu kwa vijana na kuhakikisha wanapata fursa ya kudai haki zao katika michakato ya ununuzi wa umma.

Awali akizindua Sera Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya Mwaka 2025, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba (Mb), amezielekeza mamlaka, taasisi na wadau wote wanaosimamia utekelezaji wa Sera hiyo kuhakikisha wanatekeleza majukumu yao kwa kuzingatia misingi ya utawala bora, uwazi na utawala wa sheria.‎

‎Waziri Mkuu ametoa maelekezo hayo wakati akizundua Sera hiyo kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan. Dkt. Nchemba amesema changamoto zinazoikumba sekta ya ununuzi wa umma hazitokani na sera au sheria zilizopo, bali ni uzembe na mitazamo ya baadhi ya watendaji.‎

‎Ameongeza kuwa taarifa za ukaguzi kutoka kwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) pamoja na Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA) zinaonesha wazi kuwa kasoro nyingi zinasababishwa na utekelezaji dhaifu wa sheria, kanuni na taratibu zilizopo.

“Sehemu kubwa ya changamoto hizo zinatokana na hulka, tabia na mitazamo ya watendaji. Hivyo, ni lazima tubadilike ili kufikia malengo ya sera hii,” amesisitiza Dkt. Mwigulu.

Aidha, Waziri Mkuu, amezitaka wizara, taasisi na mamlaka zote kufanya mapitio ya sera, sheria na kanuni zinazokinzana na sera hiyo ili kuweka mazingira rafiki ya utekelezaji wake.

Naye Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omar amesema sera hiyo ni mwongozo muhimu utakaosaidia kuimarisha mifumo ya ugavi katika sekta ya umma, kuongeza uwajibikaji katika matumizi ya fedha za umma na kudhibiti vitendo vya rushwa.‎
Balozi Khamis ameongeza kuwa utekelezaji wa sera hiyo utaongeza ajira, kuimarisha mnyororo wa thamani na kuchochea mageuzi makubwa ya kiuchumi kuelekea dira ya maendeleo ya mwaka 2050.
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba (Mb), akizungumza na viongozi wa Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA), wakati alipotembelea banda ya maonesho katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete, Jijini Dodoma, kabla ya kuzindua rasmi Sera Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya Mwaka 2025.Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba (Mb), (Katikati Kulia), akiwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), na viongozi wengine wakisikiliza maelezo kutoka kwa Katibu Mtendaji wa Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA), Bw. James Sando (kushoto), kuhusu mchango wa PPAA katika Mnyororo wa Ugavi, wakati Mhe. Waziri Mkuu alipotembelea banda ya maonesho katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete, Jijini Dodoma, kabla ya kuzindua rasmi Sera Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya Mwaka 2025.Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba (Mb), akizindua rasmi Sera Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya Mwaka 2025 katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete, Jijini Dodoma.
Sehemu ya viongozi mbalimbali walioshiriki katika uzinduzi wa Sera Taifa ya Usimamizi wa Mnyororo wa Ugavi ya Mwaka 2025 katika Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete, Jijini Dodoma.




 

MSIMU wa mbio za Mac D Promotions ‘ Mac D Marathon’ kwa mwaka 2026 unatarajiwa kufanyika Julai 4 mwaka huu katika viwanja vya Chuo cha Taifa cha Ulinzi (NDC,)  Kwa kauli mbiu ya ‘Go Green With Gas’ yenye kulenga kuhamasisha matumizi ya nishati safi na kutunza misitu.

Akizungumza katika uzinduzi wa mbio hizo uliofanyika katika Hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam Mkurugenzi wa Mipango na Biashara wa Mac D Promotions Denzel Rweyunga amesema kuwa mbio hizo ambazo usajili wake umeanza rasmi leo zinatarajiwa kushirikisha wakimbiaji wa Kilomita 5, 10 na 21 pamoja na mbio za watoto za Kilomita 2.

Amesema kuwa licha ya kuhamasisha utunzaji wa afya kwa kukimbia mbio hizo pia zimelenga kuunga mkono juhudi za Serikali katika kutunza mazingira kwa kuhamasisha matumizi ya nishati safi.

“Tunategemea kuwa na washiriki 3500 katika mbio hizi na maandalizi yameanza mapema ili kuzipa hadhi na viwango vya juu, na tayari usajili umefunguliwa kupitia www.macdmarathon.com na baada ya kujisajili na kufanya malipo kupitia simu au benki washiriki wataweza kupata vifaa zikiwemo tisheti katika vituo mbalimbali vilivyoainishwa.” Amesema.

Kwa undani wa taarifa hii tembelea www.michuzi.co.tz




 


Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Kanda Maalum imefanya kikao kazi na wadau wa habari, wakiwemo wamiliki, wahariri na waandishi wa habari, kwa lengo la kujenga ushirikiano endelevu kati ya taasisi hiyo na vyombo vya habari nchini.


Kikao kazi hicho kimefanyika Aprili 9, 2026 katika ukumbi wa mikutano wa Shule ya Uongozi Mwalimu Nyerere, Kibaha, mkoani Pwani.

Akifungua kikao hicho, Katibu Msaidizi wa Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Kanda Maalum, Bi. Elizabeth Komba, amesema vyombo vya habari si kioo tu cha jamii bali pia ni nyenzo muhimu ya kuunda na kukuza maadili nchini.

“Tunaamini kuwa vyombo vya habari vina nafasi ya kipekee katika kukuza maadili, uwajibikaji na uwazi katika jamii. Kwa maneno mengine, nyinyi ni nguzo muhimu katika kujenga au kubomoa maadili katika jamii. Hivyo, tutumie tasnia hii kujenga jamii yenye uadilifu,” amesema Bi. Komba.

Aidha, ameongeza kuwa vyombo vya habari vina nafasi kubwa katika kukuza uwajibikaji kwa kufichua vitendo vya rushwa, ubadhilifu na matumizi mabaya ya madaraka, kwa kuweka wazi ukweli unaowezesha wahusika kuwajibika.

“Kama tukitumia vyombo vya habari kwa njia sahihi, tunaweza kujenga jamii yenye uadilifu, uwazi na haki. Lakini tukivitumia vibaya, tunaweza kuharibu maadili, kuleta migawanyiko miongoni mwetu na hatimaye kujenga jamii isiyo na uzalendo,” alisisitiza.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Mipango, Ufuatiliaji na Tathmini kutoka Sekretarieti hiyo, Bw. Omary Juma, amesema ushirikiano huo utakuwa endelevu, huku wakiahidi kuendelea kukutana mara kwa mara ili kujadili mbinu bora za kukuza na kuimarisha maadili nchini.

Katibu Msaidizi Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Kanda Maalum Bi. Elizabeth Komba akizungmza wakati akifungua Kikao Kazi cha wamiliki, wahariri na waandishi wa habari wa Kanda hiyo. Kikao hicho kimefanyika katika ukumbi wa mikutano wa Shule ya Uongozi Mwalimu Nyerere mjini Kibaha mkoani Pwani tarehe 09 Aprili, 2026.





 


Top News