Katika juhudi za kubadili ndoto za Watanzania kuwa uhalisia, TCB Bank imezindua kampeni mpya inayolenga kuimarisha ushirikiano wa karibu na wateja wake badala ya kutoa huduma za kifedha pekee.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo uliofanyika Machi 18, 2026 jijini Dar es Salaam, Mwakilishi wa Mkurugenzi Mtendaji wa benki hiyo, Jema Msuya, amesema TCB imejipanga kuwa zaidi ya taasisi ya kifedha kwa kujikita kuwa mshirika wa kweli katika safari ya maendeleo ya mteja.

“Kwa kila azma, lengo au nia ya Mtanzania, tunatambua kuwa anastahili msaada wa stahiki. Ndiyo maana tunajitambulisha kama mshirika wa ukuaji, si tu benki,” amesema.

Ameeleza kuwa kampeni hiyo inaweka mkazo mkubwa katika uelewa wa mteja, akibainisha kuwa changamoto kubwa kwa wengi si kukosa ndoto, bali ni ukosefu wa msaada sahihi wa kifedha.

Kwa mujibu wa Msuya, TCB inaamini kuwa kumwezesha mjasiriamali mmoja kunachochea maendeleo ya jamii nzima. 

Amesema kupitia huduma zake, benki hiyo inalenga kukuza biashara ndogo na za kati, kuimarisha ustawi wa jamii na kuchangia ukuaji wa uchumi wa taifa.

Amewahimiza Watanzania kuchukua hatua za kutimiza ndoto zao kwa kushirikiana na benki hiyo.

“Ndoto yako inaanzia kwako. Sisi tupo hapa kuhakikisha inakuwa uhalisia. Karibu tushirikiane kuijenga kesho bora,” amesisitiza.

Aidha, benki hiyo imeanza mpango maalum wa kuhuisha akaunti zisizotumika, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kurejesha uhusiano na wateja na kuwapatia huduma zenye tija zaidi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Masoko na Mawasiliano wa TCB, Alex Dwashi, amesema kampeni hiyo inalenga kugusa maisha ya Watanzania kwa kuwatambua na kuwaunga mkono katika safari ya kutimiza ndoto zao.

Amefafanua kuwa kuwa na ndoto pekee haitoshi, bali kunahitajika hatua madhubuti pamoja na msaada sahihi ili kuzifanya ziwe halisi.

Ametaja mifano ya wajasiriamali wanaoanzisha na kukuza biashara, wakulima wanaoongeza uzalishaji, pamoja na familia zinazowekeza katika elimu ya watoto wao, akisisitiza kuwa maendeleo katika maeneo hayo huongeza fursa kwa jamii nzima.

Ameongeza kuwa kupitia kampeni hiyo, TCB inalenga kujenga uhusiano wa karibu zaidi na wateja wake kwa kuwauliza swali kuu, “Ndoto yako ni nini?”, ili iweze kutoa suluhisho mahsusi kulingana na mahitaji ya kila mmoja.

Aidha, amesema benki hiyo imejipanga kuhudumia makundi mbalimbali ikiwemo wafanyabiashara, wajasiriamali, wakulima na familia, huku ikipanua huduma zake katika maeneo ya uwekezaji na bima.

Amesisitiza kuwa mafanikio ya TCB yanategemea mafanikio ya wateja wake, hivyo itaendelea kuwa mshirika wa karibu katika kuchochea maendeleo ya uchumi wa taifa.








Makamu wa Pili wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdullah akiwa katika Iftari iliyoandaliwa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Zanzibar Machi 17, 2026 amesema Serikali haitawavumilia wale wote wanaokwepa Kodi kwa kujihusisha nabiashara za Magendo.

Akizungumza kwa niaba ya Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi kwenye Iftari hiyo iliyohudhuriwa na Walipakodi Visiwani Zanzibar pamoja na watumishi wa TRA katika hoteli ya Madinat Al Bahr Makamu wa Pili wa Rais SMZ Mhe. Hemed amesema vyombo vya dola vipo imara kufuatilia wanaokwepa kodi na kuchukua hatua.

Amesema Serikali ipo bega kwa bega na TRA kuhakikisha wanatimiza wajibu wao wa kukusanya kodi na kuwasaidia kupambana na wote wanaokwepa kodi maana wamekuwa wakiidhoofisha nchi kwa kuikosesha mapato.

"Hakuna unafiki kwenye masuala ya kodi, Kama unawapenda viongozi wetu wakuu lipa kodi kwa uaminifu ili kuwawezesha kutekeleza miradi ya maendeleo na kuwahudumia wananchi" amesema Makamu wa Pili wa Rais SMZ.

Aidha amesema maendeleo yanayoonekana katika kila kona ya nchi yanatokana na makusanyo ya Kodi hivyo kila mwananchi anapaswa kuchangia maendeleo hayo kwa kulipa kodi.

Akizungumza katika Iftari hiyo Kamishna Mkuu wa TRA Bw. Yusuph Juma Mwenda amesema TRA itaendelea kuwezesha biashara nchini kwa kutatua changamoto za walipakodi, kuwasikiliza na kurahisisha ulipaji kodi kwa kutumia mifumo.

Ameishukuru Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kuendelea kuwezesha mamlaka hiyo kukusanya kodi na kuboresha mazingira ya utoaji wa huduma za kodi ikiwemo elimu ya biashara na uwezeshaji biashara.








Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Bw. Yusuph Juma Mwenda amesema Mamlaka hiyo itaanzisha utaratibu mpya wa kuingiza mafuta ya kupikia Tanzania Bara kutoka Zanzibar ili kuwezesha kufanyika kwa biashara halali ya mafuta hayo na kuzuia mafuta ya magendo kuingizwa nchini.

Akizungumza na wafanyabiashara wanaoagiza mafuta ya kupikia nje ya nchi kupitia Visiwani Zanzibar na kuyasafirisha kwenda Tanzania Bara Machi 17.2026 Visiwani Zanzibar Kamishna Mkuu Mwenda amesema TRA itaanza kutekeleza utaratibu huo mpya wa utolewaji wa vibali vya kuingiza mafuta Tanzania Bara kutoka Zanzibar hivi karibuni.

Amesema utaratibu huo unalenga kurasimisha biashara ya mafuta baina ya Tanzania Bara na Zanzibar na kutoa punguzo la kodi kwa wafanyabiashara hao ili kuwawezesha kupata faida ambapo kutakuwa na kiwango maalum cha kuingiza wa mafuta hayo kulingana na mahitaji ili kulinda viwanda vya ndani.

“Lengo hapa ni kuwezesha biashara ya mafuta ya kupikia kwa kuwezesha wanaofanya biashara hiyo kufanya kwa njia halali na kujipatia kipato huku Serikali nayo ikikusanya kodi, na kupnguzo tutakalotoa siyo chini ya asilimia 70” amesema Kamishna Mkuu Mwenda.

Amesema kuanza kwa utaratibu huo kutaongeza ufanyaji kazi wa Bandari za Bagamoyo, Mbweni na Kunduchi na kuwahakikishia wafanyabiashara hao kuwa kutakuwa na uwazi katika utoaji wa vibali hivyo vya uingizaji wa mafuta ya kupikia kutoka Zanzibar kwenda Tanzania Bara.

"Niliunda Timu kwaajili ya kutafuta suluhisho la uingizaji wa mafuta ya magendo ambayo ilishirikisha wazalishaji wa ndani, waingizaji wa mafuta na wataalam kutoka TRA ambayo imekuja na mapendekezo yanayolenga kuondoa tatizo la uingizaji wa mafuta ya magendo" amesema Bw. Mwenda.

Amesema lengo la kuweka udhibiti huo ni kutaka kulinda viwanda vya ndani, kuwezesha biashara, kulinda afya za wananchi na kukusanya kodi ili kuwezesha Serikali ipate sehemu yake na Walipakodi nao wapate sehemu yao.

Akizungumza katika kikao hicho Mfanyabiashara wa mafuta ambaye huagiza kutoka nje ya nchi Hassan Said Ngozi amemshukuru Kamishna Mkuu wa TRA na kuipongeza Mamlaka hiyo kwa kuja na uamuzi huo utakaowezesha kuendelea kwa biashara zao maana walisimama kusafirisha ili kusubiri muongozo.







-Waziri: Hekta 158,000 za hifadhi zilindwe, ziwe ngao ya mabadiliko ya tabianchi

Na Mwandishi Wetu, Lindi

WAZIRI wa Maliasili na Utalii, Mhe Dkt. Ashatu Kijaji, amezindua kwa vitendo kampeni ya kitaifa ya upandaji miti kwa kupanda mikoko 1,020 katika fukwe za Machole, mkoani Lindi, akisisitiza umuhimu wa kulinda zaidi ya hekta 158,000 za misitu ya mikoko nchini kama nguzo ya uchumi na kinga dhidi ya mabadiliko ya tabianchi.

Akizungumza leo Machi 18, 2026 katika tukio la Siku ya Mikoko, moja ya matukio ya awali kuelekea kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Misitu Duniani yatakayofanyika Machi 21, Waziri Kijaji alisema Tanzania imebarikiwa kuwa na mikoko kuanzia Tanga hadi Mtwara, lakini uhifadhi wake unahitaji ushirikiano wa wadau wote.

“Mikoko ni muhimu kwa uchumi na uhai wa dunia. Ina uwezo mkubwa wa kufyonza hewa ukaa kuliko aina nyingine nyingi za misitu, hivyo ni silaha muhimu katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi,” alisema.

Aliongeza kuwa mbali na kuchangia kupunguza athari za tabianchi, mikoko ni mazalia ya samaki na viumbe wengine wa baharini, hivyo uharibifu wake ni tishio kwa usalama wa chakula na uchumi wa jamii za pwani.

“Mikoko inalinda fukwe dhidi ya mmomonyoko kwa kupunguza nguvu ya mawimbi. Maeneo yenye mikoko imara hayakabiliwi na mmomonyoko mkubwa,” alisisitiza.

Katika tukio hilo lililoshirikisha viongozi wa serikali, wadau wa mazingira na wananchi, Waziri huyo aliupongeza Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) kwa kazi ya kusimamia na kulinda rasilimali hiyo, akitoa wito wa kuendeleza juhudi hizo sambamba na kampeni ya kitaifa ya upandaji miti iliyoanzishwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan chini ya ajenda ya “Tanzania ya Kijani.”

Aidha, aliwataka wananchi wa Lindi na mikoa jirani kujitokeza kwa wingi katika ufunguzi wa maadhimisho hayo utakaofanyika kesho Machi 19, 2026 katika Uwanja wa Ilulu, yakitarajiwa kufunguliwa na Makamu wa Rais wa Tanzania, Mhe Dk Emmanuel Nchimbi.

Kwa upande wake, Kamishna Msaidizi wa Uhifadhi na Kaimu Mkurugenzi wa Usimamizi wa Rasilimali TFS, Dkt. Zainabu Shaban Bungwa, alisema mikoko ina spishi tisa zinazotambulika kitaalamu nchini, huku akibainisha kuwa mti uliopandwa na Waziri ni Rhizophora mucronata, maarufu kama mkoko.

Alieleza kuwa mikoko ina uwezo mkubwa wa kufyonza hewa ukaa ambapo hekta moja inaweza kunyonya kati ya tani 800 hadi 1,200 za hewa ukaa, kiwango kinachozidi mara kadhaa miti ya kawaida inayonyonya kati ya tani 160 hadi 300.

Akitoa maelezo ya kitaalamu, Mhifadhi Mkuu mstaafu wa TFS ambaye kwa sasa ni Meneja wa Mradi wa BENGO, Frank Sima, aliyewasilisha kwa niaba ya Katibu wa Sekretarieti ya Mtandao wa Mikoko wa Ukanda wa Magharibi mwa Bahari ya Hindi (WIOMN), alisema katika tukio hilo zilipandwa spishi nne za mikoko ambazo ni Rhizophora mucronata, Avicennia marina (mchu), Bruguiera gymnorhiza (msinzi) na Ceriops tagal (mkandaa).

Alibainisha kuwa upandaji huo umefanyika kwa kufuata viwango vya kitaalamu kwa kutumia nafasi ya mita mbili kwa mbili katika mfumo wa zigzag ili kuongeza ufanisi wa ukuaji, ukihusisha eneo la takriban hekta 0.5.

Tukio hilo pia lilihudhuriwa na viongozi wa Mkoa na Wilaya ya Lindi wakiongozwa na Mkuu wa Wilaya, Mkuu wa Wilaya ya Lindi, Mhe Victoria Mwanziva, Mbunge wa Mchinga, Mhe Salma Kikwete pamoja na wadau wa kimataifa wa uhifadhi wakiwemo IUCN, taasisi ya Mwambao Coastal Community Network, EarthLung na wadau wa maendeleo ya Bahari ya Hindi.

Maadhimisho ya mwaka huu yanafanyika wakati Tanzania ikiendeleza mikakati ya kimataifa ya uhifadhi na urejeshaji wa misitu, ikilenga kuongeza uoto wa asili, kulinda bioanuai na kuchochea uchumi wa kijani kupitia utalii wa mazingira na rasilimali misitu.










Na Diana Byera,Bukoba

MBUNGE wa Jimbo la Bukoba Mjini, Johnston Mutasingwa ameendelea kugusa maisha ya wananchi kwa vitendo baada ya kutoa msaada kwa makundi maalum pamoja na wanufaika wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF)  katika Kata ya Kibeta katika kipindi iki cha Mfungo wa Kwalezima na Ramadhan

Msaada huo umekabidhiwa leo Machi 18,2026  kupitia Katibu wake Hamada Simba ambaye amesema  Mbunge kwa sasa yupo nje ya jimbo akiendelea na majukumu ya ubunge lakini  bado anawajali wananchi wake na kuhakikisha wanapata msaada wa  mahitaji katika kipindi hiki Cha Mfungo 

Amesema msaada huo unalenga kuwasaidia wananchi walio katika mazingira magumu, wakiwemo wazee, watu wenye ulemavu pamoja na kaya zenye kipato cha chini zinazofaidika na mpango wa TASAF.

Mahitaji yaliyotolewa ni pamoja na chakula sukari Sabuni na Vyakula mbalimbali vya kusaidia katika  familia hizo katika Mfungo.

Kwa upande wao wananchi ambao wamenufaika na msaada huo wameonesha furaha na kutoa shukrani zao za dhati kwa Mbunge wao, wakieleza kwamba hatua hiyo imewapa faraja kubwa na kuwasaidia kukabiliana na changamoto za maisha ya kila siku.

“Tunamshukuru sana Mheshimiwa Mbunge kwa kutujali,Msaada huu umekuja wakati sahihi na utatusaidia sana katika maisha yetu,” amesema mmoja wa wanufaika.

Wakati huo huo Diwani wa Kata kibeta  AnaStella Alphuns amesema kwa ujumla, tukio hilo limeendelea kuonesha mshikamano kati ya viongozi na wananchi pamoja na juhudi zinazoendelea za kuhakikisha ustawi wa jamii unaimarika, hasa kwa makundi yenye uhitaji zaidi.








 

Na Mwandishi Wetu, Lindi

Fursa ya biashara ya kaboni imeelezwa kuwa mkombozi mpya wa uchumi wa misitu nchini, huku Serikali ikihimiza wananchi na wadau kuchangamkia rasilimali hiyo kwa manufaa ya kiuchumi na uhifadhi wa mazingira.

Hayo yamebainishwa Machi 18, 2026 katika Uwanja wa Ilulu, Manispaa ya Lindi, wakati wa Jukwaa la Majadiliano ya Biashara kwa Biashara (B2B) lililoandaliwa kama sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Misitu Duniani na kampeni ya kitaifa ya upandaji miti.

Akiwasilisha mada kuhusu biashara ya kaboni, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi na Meneja wa Baiolojia ya Mbegu za Miti kutoka TFS, Fandey Mashimba, amesema biashara hiyo ni fursa kubwa ya kiuchumi unaowezesha nchi kama Tanzania kunufaika kwa kuhifadhi misitu au kupanda miti ambayo husaidia kufyonza gesi joto ya  CO₂.

Amesema biashara ya kaboni ilianzishwa kimataifa ili kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi yanayosababishwa na ongezeko la gesi joto, huku nchi zilizoendelea zikitakiwa kulipia juhudi za nchi zinazoendelea katika kuhifadhi mazingira kwa kufyonza gesijoto ikiwemo  CO₂ kupitia misitu na sekta nyingine.

“Misitu yetu ni hazina kwa sababu inafyonza gesijoto ambapo kutokana na hilo viwango vya kaboni (carbon credits) hupatikana na kuuzwa. Amefafanua, tani 1 ya CO₂ iliyo fyonzwa kwa mwaka na mimea au kiasi hichohicho cha gesi joto kilichozuiwa kusambaa hewani ndio huuzwa kama kiwango cha Kaboni kulingana na mradi na uthibitisho baada ya upimaji.

 Tukisimamia vizuri na kuwa na takwimu sahihi, tunaweza kuuza kaboni ( ‘carbon credits’) na kupata mapato,” amesema Mashimba.

Amefafanua katika biashara hiyo hakuna ardhi, msitu, miti au rasilimali yeyote inayouzwa au wananchi kunyang'anywa ardhi (land grabbing) bali mwekezaji huwa ana haki na viwango vya kaboni tu vilivyo zalishwa wakati wa uwekezaji kinyume na taarifa potofu ambazo zimekuwa zikibeza biashara ya Kaboni. 

Amesema, bidhaa ya kaboni ni sawa na bidhaa nyingine na pia zina masoko yake  kwenye soko la kimataifa na kama nchi tayari kuna kanuni na muongozo chini ya sheria ya mazingira inayo simamiwa na Ofisi ya Makamu wa  Rais, Mazingira.

Hata hivyo, amesema wananchi wengi bado wana hofu na uelewa mdogo kuhusu biashara hiyo, akisisitiza umuhimu wa elimu na uwekezaji katika tafiti na mifumo ya upimaji wa kaboni ili kuondoa hofu.

Akichangia mada hiyo, Mbunge wa Jimbo la Mchinga Mkoani Lindi na Mke wa Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne, Mhe Salma Kikwete, amesema kuna haja ya kutoa elimu kwa wananchi ili waweze kuelewa thamani ya misitu na kuepuka uharibifu unaotokana na matumizi ya nishati kama mkaa.

Katika wasilisho jingine ambalo limetambulisha miti mingine ambayo haijulikani lakini baada ya utafiti imeonekana kufaa katika matumizi ya mbao, amesema pamoja na ongezeko la thamani ya miti ya asili, wananchi wengi huuza mazao ya misitu kwa bei ndogo kutokana na ukosefu wa taarifa sahihi za soko na thamani halisi ya rasilimali hizo na kuomba elimu itolewe ili wananchi wanufaike na misitu yao.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Mhe Zainab Telack, ameitaka Wizara ya Maliasili na Utalii kuweka mazingira rafiki yatakayowawezesha wananchi wengi kushiriki katika biashara ya kaboni.

Amesema mkoa huo una vijiji zaidi ya 70 vyenye misitu ya hifadhi vinavyoweza kunufaika na biashara hiyo endapo vitapewa elimu na miongozo sahihi.

Mhe Telack pia ameshauri vibali vya uvunaji wa misitu viambatane na masharti ya upandaji miti ili kuhakikisha uendelevu wa rasilimali hizo kama inavyo fanyika kwa watumiaji wa miti wanapo sindika tumbaku.

Jukwaa hilo limejadili mada nane muhimu ikiwemo biashara ya kaboni, matumizi ya teknolojia, sera na kanuni pamoja na namna ya kuongeza thamani ya mazao ya misitu.

Kesho Machi 19, 2026, uzinduzi rasmi wa maadhimisho ya Siku ya Misitu Duniani na Kampeni ya Upandaji Miti Kitaifa unatarajiwa kufanywa na Makamu wa Rais, Mhe Emmanuel Nchimbi, huku Serikali ikiendelea kusisitiza kaulimbiu ya mwaka huu: “Misitu ni Uchumi Endelevu, Tuihifadhi kwa Maendeleo ya Taifa.”

















Top News