Naibu Waziri wa Kilimo Mhe David Silinde amesema kuwa Serikali imeweka dhamira ya kuleta mabadiliko katika sekta ya kilimo ili kupunguza umaskini na kuongeza ajira hasa kwa vijana na wanawake na kufikia asilimia 10 ya ukuaji wa kilimo ifikapo mwaka 2030.
Mhe Silinde ameyasema hayo leo Jijini Dodoma Machi 3,2026 wakati akifungua Mkutano wa nne wa Kitaifa wa Kilimo ikolojia hai, akimuwakilisha Waziri wa Kilimo Mhe Daniel Chongolo.
Ambapo amesema Serikali imechukua hatua za kuleta mabadiliko hayo katika sekta ya kilimo ikiwa ni pamoja na kuongeza bajeti ya Wizara kufikia trilioni 1.24 kwa 2025/2026.
"Ndugu Washiriki, nipende kuwajulisha kwamba Serikali imedhamiria kwa dhati kabisa kuleta mabadiliko makubwa katika sekta ya Kilimo ili kuchangia katika kupunguza umaskini, kuongeza ajira hususani kwa vijana na wanawake na kufikia asilimia 10 ya ukuaji wa kilimo ifikapo mwaka 2030. Katika jitihada za kuleta mabadiliko hayo, Serikali imechukua hatua mahsusi katika sekta ya kilimo ikiwa ni pamoja kuongeza bajeti ya kilimo kufikia trilioni 1.24 mwaka 2025/2026".
Aidha ameeleza kuwa Mkutano huu uliohudhuriwa na wadau kutoka ndani na nje ya Tanzania, unalenga kutafakari kwa kina namna ya kuendeleza jitihada mbalimbali za Kilimo Ikolojia Hai ikiwemo utekelezaji wa Mkakati wa Kilimo Ikolojia Hai wa 2023-2030 lengo ikiwa ni kuhakikisha kuwa viashiria vya mipango ya maendeleo ikiwemo Mpango Kabambe wa Kilimo (Agriculture Master Plan), Mpango Jumuishi wa Maendeleo ya Kilimo Afrika (CAADP), Dira ya Maendeleo na Malengo Endelevu ya Maendeleo (SDGs) vinatekelezwa kufikia utoshelevu wa chakula nchini kwa kuzingatia lishe bora na utunzaji wa mazingira.
Na kuongeza kuwa katika kutekeleza maazimio ya mkutano wa Tatu wa Kilimo Ikolojia Hai uliofanyika mwaka 2023, Serikali imetenga fedha kwenye bajeti ya Wizara ya mwaka 2025/26 kwa ajili ya utekelezaji wa Mkakati wa vyuo kuanza kufundisha Kilimo Ikolojia, mfano Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine (SUA). na Wizara kufanya jitihada mbalimbali za kutunza mbegu za asili kupitia Taasisi ya Utafiti wa Kilimo kwa kukusanya, kusafisha na kuhifadhi jumla ya mbegu za asili 770 za mazao ya ulezi, mpunga, mtama, uwele, migomba, maharage na papai,
Ambapo Wizara kupitia TOSCI tayari imekamilisha utambuzi wa aina 13 za mbegu za asili za mahindi, mpunga, maharage na papai ambazo zimeingizwa kwenye mfumo rasmi wa mbegu.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Mwamvuli wa kilimo hai(TOAM) Dkt Mwatima Juma amesema kuwa huu ni Mkutano wa wadau kukumbushana, kuwapa nafasi za kuwa na maudhui mbalimbali ya kisayansi,ya kijamii na ya maendeleo ambayo yatazungumzwa na watu kupata nafasi ya kujadiliana.
Na kusema kuwa kilimo hai kinakwenda mbio sana duniani hivyo nao wanatakiwa kukaza kamba kukisukuma kiende mbio zaidi kutokana na mujibu wa masoko.
Naye Mkurugenzi Mkuu wa mwamvuli wa Kilimo hai (TOAM) Bwana Bakari Mongo ameeleza kuwa Mkutano huu huwa ni jukwaa muhimu sana kwa wadau mbalimbali wakiwemo wakulima,watafiti,wanazuoni,Wana Habari,Sekta binafsi na pia wabia wa Maendeleo kubadilishana maarifa na uzoefu ambao utasaidia kuendeleza kilimo Ikolojia Hai katila Taifa la Tanzania.
Kwani katika Mkutano wao huu wa nne wanategemea kuwa na maazimio lakini pia kujipima walipofikia juu ya yale ambayo walikubaliana katika mikutano iliyopita na kuweka maazimio tena yanayolenga zaidi kusukuma gurudumu la kilimo Ikolojia hai katika Taifa.
Awali wakitoa ushuhuda wa mafanikio ya kilimo hai Bwana Manase Noeki kutoka Halmashauri ya Arusha DC amesema kilimo cha Ikolojia hai kimempa manufaa makubwa ikwemo kuendana na mabadiliko ya Tabia nchi na pia namna ya kutunza mazingira kama vile kuweka kingo,kuotesha miti,kuotesha majani na kutumia mbolea za mifugo kwaajili ya kutunza afya ya udongo.
Naye Bi Mercy Meena mkulima kutoka Morogoro amesema kilimo hiki kimemsaidia kulima mazao mbalimbali ambayo yalisemwa hayatostawi katika maeneo yao lakini kwa kufuatilia kilimo Ikolojia hai alikuta yote yakistawi na akitumia mbegu za asili.
Mkutano huu ni wa siku tatu na unaongozwa na kauli mbiu inayosema “Kilimo Ikolojia Hai: Kuimarisha Usalama wa Chakula na Lishe, Uhimilivu na Ustahimilivu wa Kiuchumi”.
.jpeg)