Waziri wa maliasili na utalii Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) leo tarehe 10 julai, 2026 amekutana na bodi ya wakurugenzi mamlaka ya hifadhi ya Ngorongoro katika ofisi za mamlaka hiyo zilizopo Karatu mkoani Arusha na kusisitiza umuhimu wa bodi hiyo kufuatilia kwa karibu shughuli zote za utendaji ili kuanza mwaka mpya wa fedha 2026/2027 kwa kasi na ufanisi.

Mhe. Kijaji amesema kuwa bajeti ya mwaka mpya wa fedha inaanza na utekelezaji wa dira ya taifa ya maendeleo ya mwaka 2050 hivyo vikao vyake na bodi za taasisi zilizopo chini ya wizara vina lengo la kuanza utekelezaji wa dira, bajeti na ilani ya Chama cha Mapinduzi kwa pamoja.

Ameitaka bodi hiyo kuongeza nguvu katika kuimarisha uhifadhi, kutangaza utalii na kusimamia maendeleo ya jamii na kusisitiza kuwa jitihada hizo ziendane na kasi ya kukamilisha miundombinu wezeshi ikiwemo barabara kuu ya Loduare hadi Golini, kuimarisha mawasiliano ndani ya eneo lote la hifadhi, kukamilisha mradi wa fensi ya umeme ili kupunguza migongano kati ya wanyamapori na wananchi, kudhibiti ujangili na kuendelea kuimarisha mahusiano ya hifadhi na wananchi wanaoizunguka.

“Tulinde uhifadhi wa Ikolojia ya Ngorongoro kwa wivu mkubwa, tuendelee kubuni mazao mapya ya utalii na kuyatangaza, tujipange kikamilifu kuhakikisha Ngorongoro kama premium destination inawafikia na kuwashawishi wageni watakaohudhuria matukio ya AFCON, mkutano wa umoja wa Mabunge duniani, tuzo za dunia za utalii na shindano la Miss world ambapo matukio yote yatafanyika Tanzania kati ya mwezi oktoba 2026 na Julai mwaka 2027” amesisitiza Dkt. Kijaji.

Katibu wa Bodi, ambae ni kamishna wa Uhifadhi Ngorongoro Abdul-Razaq Badru amemueleza Mhe. waziri kuwa, Ngorongoro imepiga hatua ya kimageuzi kwenye mifumo ya kidijitali (ICT Transformation), uhifadhi endelevu kwa kuimarisha doria za kisasa, kuboresha miundombinu hasa barabara ya tabaka gumu kutoka geti la loduare hadi Seneto (km 29.5) kwa gharama ya TZS 80.3 bilioni

Badru ameongeza kuwa katika mwaka wa fedha 2025/26 eneo la Ngorongoro idadi ya watalii ilifikia 1,061,620 na fedha shilingi 269.5 Bilioni zilikusanywa. Ngorongoro imeendelea na jitihada za kulinda hadhi tatu za kimataifa kutoka UNESCO ambazo ni Urithi wa Dunia (World Heritage Site), Hifadhi ya Biosphere (Man and Biosphere Reserve), na Geopark ya Dunia (Ngorongoro-Lengai Global Geopark) ili ziendelee kuinufaisha nchi yetu.

Kwa upande wake makamu mwenyekiti wa Bodi ya wakurugenzi Ngorongoro Dkt. Harriet Mtae amemueleza Mhe waziri kuwa, katika kipindi cha miezi sita (06) iliyopita bodi ya Ngorongoro imetekeleza majukumu kwa kuzingatia sheria, kanuni pamoja na maelekezo ya Serikali ili kuhakikisha Mamlaka inatekeleza kikamilifu dhamana yake ya kuhifadhi maliasili za Wanyamapori, malikale na urithi wa dunia, kuendeleza utalii endelevu na kuboresha shughuli za maendeleo ya jamii.



Na Janeth Raphael MichuziTv

Vigogo wanane wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT) wameendelea kushikiliwa rumande baada ya upande wa Jamhuri kueleza kuwa upelelezi wa kesi ya uhujumu uchumi na rushwa inayowakabili bado haujakamilika.

Shauri hilo lilipotajwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Dodoma jana, Julai 9, 2026, Wakili wa Serikali, Gothard Mwingira, aliiambia mahakama kuwa upelelezi umefikia hatua za mwisho, lakini bado haujakamilika. Alieleza kuwa upande wa mashtaka unasubiri kibali cha Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) kabla ya kuendelea na hatua zinazofuata za shauri hilo.

Kutokana na maelezo hayo, upande wa Jamhuri uliomba mahakama ipange tarehe nyingine kwa ajili ya kutajwa kwa kesi hiyo wakati taratibu za upelelezi zikikamilishwa.

Washtakiwa katika shauri hilo ni aliyekuwa Rais wa CWT, Leah Ulaya, Rais wa sasa wa CWT, Suleiman Ikomba, aliyekuwa Katibu Mkuu wa chama hicho, Maganga Japhet, Katibu Mkuu wa sasa, Joseph Misalaba, pamoja na Nashon Kidudu, Baraka Mbonalibha, Wambura Kihengu na Angelina Wambura. Pia kampuni ya Pyrite and Industries Company Limited inatajwa kama mshtakiwa katika kesi hiyo.

Viongozi hao walifikishwa kwa mara ya kwanza mahakamani Mei 25, 2026, ambapo walisomewa jumla ya mashtaka 14 yanayohusisha uhujumu uchumi na rushwa.

Hata hivyo, hawakutakiwa kujibu mashtaka hayo kwa kuwa Mahakama ya Hakimu Mkazi haina mamlaka ya kusikiliza kesi zinazohusu uhujumu uchumi.

Shauri hilo litaendelea kutajwa mahakamani baada ya upande wa Jamhuri kukamilisha upelelezi na kupata kibali kinachohitajika kutoka kwa Mkurugenzi wa Mashtaka.





New York, Marekani


Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeeleza hatua zake za kuanza kutekeleza Mpango wa Nne wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano, 2026/27–2030/31 (FYDP IV), ambao ni mpango wa kwanza wa muda wa kati wa kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Hayo yamelezwa na Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais–Mipango na Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Mipango, Dkt. Tausi Mbaga Kida, wakati wa mkutano wa pembezoni mwa Jukwaa la Ngazi ya Juu la Siasa la Umoja wa Mataifa linalosimamia Utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo Endelevu (HLPF 2026), uliofanyika katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, New York, Marekani.

Mkutano huo, wenye mada “Driving Industrial and Inclusive Economic Transformation: Financing, Innovation and Sustainable Growth in Agricultural and Blue Economy Value Chains”, uliandaliwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushirikiana na Mfuko wa Umoja wa Mataifa wa Maendeleo ya Mitaji (UNCDF), pamoja na UNDP, UNIDO na washirika wengine.

Dkt. Kida alisema Tanzania inaingia katika awamu mpya ya utekelezaji wa maendeleo inayolenga kubadilisha mafanikio ya ukuaji wa uchumi na uwekezaji katika miundombinu kuwa ongezeko la uzalishaji, ajira zenye tija, mauzo ya nje, ongezeko la thamani ya bidhaa na ustawi mpana wa wananchi.

Dkt. Kida alisema uchumi wa Tanzania kwa sasa unakua kwa asilimia 5.9 na unatarajiwa kufikia asilimia 6.3 ifikapo mwisho wa mwaka huu. Ukuaji huo ulichangiwa na kuimarika kwa shughuli mbalimbali za uzalishaji na huduma, pamoja na kuendelea kwa uwekezaji katika miundombinu na miradi ya kimkakati.

Hata hivyo, alisisitiza kuwa lengo si kasi ya ukuaji pekee, bali ukuaji unaogusa maisha ya wananchi wote. “Lengo letu si kuongeza ukubwa wa uchumi pekee. Tunataka ukuaji unaoongeza kipato cha wananchi, unaotengeneza ajira, unaopunguza umaskini na unaowezesha wanawake, vijana, wakulima wadogo na wajasiriamali kushiriki kikamilifu katika uchumi,” alisema Dkt. Kida.

Dkt. Kida alibainisha kuwa kilimo, misitu na uvuvi vinaendelea kuwa sehemu muhimu ya uchumi wa Tanzania, vikichangia asilimia 24.3 ya Pato la Taifa mwaka 2025. Alisema mchango wa uvuvi katika Pato la Taifa uliongezeka kutoka asilimia 1.9 mwaka 2020 hadi asilimia 2.2 mwaka 2025, hatua inayoonesha fursa zinazoongezeka katika uchumi wa buluu.

“Tunataka kuondoka katika uchumi unaouza malighafi na kuelekea uchumi unaosindika, unaoongeza thamani, unaotumia teknolojia na unaounganisha wazalishaji wa ndani na masoko ya kitaifa, kikanda na kimataifa,” alisema.

Dkt. Kida pia alisema Tanzania itawasilisha Mapitio ya Tatu ya Hiari ya Nchi ya utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo Endelevu tarehe 14 Julai 2026.

Mapitio hayo yanaonesha maendeleo yaliyopatikana katika maji safi, nishati, miundombinu, afya, usafiri, teknolojia ya kidijitali na uimarishaji wa rasilimali za ndani.

Kwa upande wake, Balozi na Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, New York, Mhe. Togolani Edriss Mavura, alisema mageuzi ya viwanda barani Afrika yanapaswa kuwa jumuishi na kuwanufaisha wakulima wadogo, wanawake, vijana, wavuvi, wafugaji, biashara ndogo na washiriki wa sekta isiyo rasmi.

Alisisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano wa kikanda na kimataifa katika teknolojia, uwekezaji, masoko, ujuzi, fedha za maendeleo na ujenzi wa minyororo ya thamani inayounganisha nchi za Afrika.

Ofisa Mkuu wa Fedha wa UNCDF, Bw. Karen Vardanyan, aliitaja Tanzania kuwa miongoni mwa nchi zinazoonesha namna fedha bunifu zinavyoweza kutumika kuharakisha maendeleo katika ngazi ya taifa na mamlaka za serikali za mitaa.

Alieleza kuwa upatikanaji wa nishati safi ya kupikia umeongezeka kutoka asilimia 6.9 mwaka 2021 hadi asilimia 28.6 mwaka 2025. Maendeleo hayo yanaungwa mkono na utekelezaji wa Mkakati wa Taifa wa Nishati Safi ya Kupikia, uwekezaji wa sekta binafsi na juhudi za Serikali za kupunguza utegemezi wa kuni na mkaa.

Bw. Vardanyan pia alitaja Tanga UWASA Green Revenue Bond, iliyokusanya dola za Marekani milioni 20.8 kwa ajili ya miundombinu ya maji inayohimili mabadiliko ya tabianchi. Hatifungani hiyo ilikuwa ya kwanza ya kijani katika ngazi ya mamlaka ya chini ya kitaifa Afrika Mashariki, huku wawekezaji wa ndani wakichangia asilimia 65 ya uwekezaji wote.

Mifano mingine iliyotajwa ni PesaTech Accelerator, inayosaidia ubunifu wa huduma za kifedha na biashara zinazoongozwa na vijana, pamoja na mfumo wa LoCAL unaowezesha mamlaka za serikali za mitaa kuongeza uwekezaji unaohimili athari za mabadiliko ya tabianchi.

Bw. Vardanyan alitoa wito kwa Serikali, taasisi za fedha, sekta binafsi na washirika wa maendeleo kubadili ahadi za kimataifa kuwa miradi inayoweza kufadhiliwa na uwekezaji halisi katika kilimo, uchumi wa buluu, viwanda, maji, nishati na miundombinu.

Mkutano huo ulihitimisha kuwa utekelezaji wa Dira 2050 na FYDP IV utahitaji ushirikiano madhubuti kati ya Serikali, sekta binafsi, taasisi za fedha, Umoja wa Mataifa, washirika wa maendeleo, asasi za kiraia na jamii.

Dira 2050 inalenga kuifanya Tanzania kuwa nchi yenye uchumi wa kipato cha kati cha juu, yenye Pato la Taifa la dola za Marekani trilioni moja, pato la wastani kwa mtu linalozidi dola 7,000 na kuondoa umaskini ifikapo mwaka 2050.










Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Hemed Suleiman Abdulla, amesema kitabu cha 'Falsafa ya Sheria ya Mama Samia' kinaakisi mchango mkubwa wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuimarisha utawala wa sheria kwa ajili ya kuleta maendeleo. 

Amesema hayo leo wakati akizindua kitabu hicho katika ukumbi wa Maktaba ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, akimwakilisha Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba. Abdulla pia amewataka Watanzania kuendelea kudumisha amani na mshikamano. "Bila amani, maendeleo hayatafanyika. Nawaomba wale wenye mawazo tofauti waungane na Watanzania wengine kuwa wazalendo na kulinda amani ya nchi yetu," amesema.

Akizungumzia maudhui ya kitabu, Abdulla amesema waandishi wake wamekitazama sheria kama mfumo unaogusa uchumi wa jamii nzima na sio kwa upana mdogo. Amesisitiza kuwa kitabu kimegusa maeneo matatu muhimu. La kwanza ni mapato ya ndani ambayo yameongezeka kwa kiasi kikubwa kipindi cha awamu ya sita, na kusaidia serikali kugharamia miradi ya barabara, reli, umeme na afya. 

La pili ni mageuzi ya VAT na kodi nyingine ambapo mapato yameongezeka na kuonesha kodi zinaendana na uchumi wa kidigitali. La tatu ni uwekezaji ambapo maboresho ya Sheria ya Uwekezaji ya 2022 yamerahisisha huduma na kuondoa urasimu. "Serikali ya awamu ya sita inataka uwekezaji unaozalisha ajira, unaoongeza teknolojia na ushiriki wa Watanzania katika uchumi," amesema Abdulla.

Kwa upande wake, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Hamza Johari, amesema kitabu hicho kinaonesha jinsi sheria ilivyo chombo cha kuimarisha uchumi wa taifa na si cha udhibiti tu. "Sheria si maandishi tu bali ni miundombinu ya taifa. Ikiandikwa vibaya inaweza kuchelewesha maendeleo, ikiwa na utata inaleta migogoro, na ikiwa dhaifu inaleta matumizi mabaya ya mamlaka," amesema. 

Johari amemshukuru Rais Samia kwa kuendelea kuongoza nchi kwa mwelekeo wa maridhiano ili mageuzi ya uchumi, usawa na maendeleo yaweze kufikiwa.





Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Daktari (Dkt) Jakaya Mrisho Kikwete amekutana na kufanya mazungumzo na Ban Ki-moon, aliyekuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN) kuhusu kukuza elimu ya awali na msingi duniani kupitia Taasisi ya Kimataifa inayoshughulikia Masuala ya Elimu Duniani Global Partnership for Education - (GPE).

Mazungumzo hayo yamefanyika leo Seoul, Korea Kusini ikiwa ni sehemu ya ziara ya kikazi ya Dkt. Kikwete anayoifanya nchini humo kwa nafasi yake ya Mwenyekiti wa Bodi ya Taasisi ya GPE ambapo kakutana na Viongozi wa Serikali ya Korea pamoja na mashirika wadau wa GPE kwa lengo la kuimarisha ushirikiano baina ya (GPE) na wadau wa nchi za mashariki ya mbali, hususan Korea Kusini na Japan.

Katika mazungumzo yake na Ban Ki-moon, ambaye kwa sasa ni Mwenyekiti wa Taasisi za The Ban Ki-moon Foundation yenye makao yake makuu Vienna nchini Austria, na Ban Ki-moon Foundation for a Better Future yenye makao yake makuu Seoul, Korea Kusini, Rais Mstaafu Dkt. Kikwete amempongeza Katibu Mkuu huyo Mstaafu wa UN kwa kazi nzuri anayoendelea kuifanya kupitia Taasisi zake ya kuhamasisha ufikiwaji wa Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs), hususan Lengo Namba 4 linalohusu Elimu Bora kwa Wote, Lengo Namba 13 linalohusu Kuchukua Hatua dhidi ya Mabadiliko ya Tabianchi, na Lengo Namba 17 linalohusu Ushirikiano wa Kimataifa kati ya Serikali, Sekta Binafsi na Asasi za Kiraia katika kutimiza malengo ya SDG.

Dkt. Kikwete alitumia fursa hiyo pia kumshukuru Bw. Ban Ki-moon kwa msaada wake anaoutoa kwa Taasisi ya GPE uliowezesha kuimarika kwa mahusiano kati ya Taasisi hiyo ya GPE na Serikali ya Korea Kusini. Kwa mujibu wa taarifa inayopatikana kwenye tovuti ya GPE, Korea Kusini ni moja ya nchi na mashirika wafadhili 33 (donor countries organisation) wa GPE ambayo tangu mwaka 2015 imeshachangia jumla ya Dola za Kimarekeni milioni 20 kwa Taasisi hiyo.

Aidha Bw. Ban Ki-moon amemhakikishia Dkt. Kikwete kuwa ataendelea Taasisi zake zitaendelea kufanya kazi kwa karibu na Taasisi ya GPE, Serikali ya Korea na mashirika mengine ya kimataifa katika kukuza elimu duniani, hususan kwa watoto wanaoishi katika mazingira magumu. Katika mazungumzo yao, Bw. Ban Ki-moon alisisitiza umuhimu wa elimu katika kufungua fursa za kila mtoto duniani, huku akitoa mfano wa namna elimu bora imekuwa ufunguo katika maisha yake akieleza namna kijiji chake kiliteketezwa na moto katika Vita ya Korea ya mwaka 1950 - 1953 ambapo walilazimika kusomea chini ya mti, na kwamba ufadhili wa chakula na elimu uliotolewa na Umoja wa Mataifa ndiyo uliokoa maisha yake na kumuandaa kuja kuwa kiongozi mkubwa duniani.

Kwa upande mwingine, Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Kikwete alikutana na Viongozi mbalimbali wa Serikali ya Korea Kusini wakiwemo Makamu wa Pili wa Waziri wa Mambo ya Nje, Kim Jina, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje anayeshughulikia Ushirikiano wa Kimataifa, Chang Wook-jin pamoja na Wabunge Jae Jung Lee, Kyung-sook Kang na Geong Kim wanaohusika na masuala ya elimu na ushirikiano wa maendeleo ya kimataifa ya Korea Kusini.

Dkt. Kikwete ametumia fursa ya kukutana na Viongozi hao kuishukuru Serikali ya Korea Kusini kwa kuendelea kufanya kazi kwa karibu na Taasisi ya GPE, si tu kwa kutoa ufadhili wa kifedha, bali pia kwa kutoa uzoefu wake katika kuendeleza sekta ya elimu kwa nchi nyingine duniani, huku nchi hiyo ikisifika kwa viwango vya juu vya elimu ya hisabati, sayansi na ubunifu.

Kwa upande wao, pamoja na mambo mengine, Viongozi hao walieleza nia ya Serikali ya Korea kudumisha ushirikiano huo na kwamba inanuia kutangaza kuongeza kiwango cha fedha inachotoa kufadhili GPE katika Mkutano wa Ahadi (Replenishment Summit) utakaofanyika pembezoni mwa Mkutano wa 81 wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa (UNGA), New York, tarehe 23 Septemba, 2026.

Taasisi ya Ushirikiano wa Kimataifa kwa Elimu (GPE) imelenga kutumia Mkutano huo wa New York, Marekani kuzindua Kampeni ijulikanayo kama GPE 2030 ambapo jumla Dola za Marekani bilioni 15 zinatarajiwa kukusanywa kati ya mwaka 2026 - 2030 ili kugharamia elimu ya awali na msingi kwa watoto takribani milioni 750 katika nchi zaidi ya 90 kote duniani ikiwemo Tanzania.

Tanzania ni moja ya nchi wanufaika wa fedha zinazotolewa na Taasisi ya GPE ambapo hadi sasa imeshapokea zaidi ya Dola za Marekani milioni 207.3 kwa ajili ya kuboresha sekta ya elimu nchini. Inatarajiwa kuwa kiasi hicho cha fedha kinachotolewa kwa Tanzania kitaogezeka kupitia mpango wa GPE wa kuziongezea fedha za ufadhili nchi zinazofanya vizuri katika kusimamia sekta ya elimu ya miradi inayotekelezwa kwa ubia kati ya Serikali na Taasisi ya GPE.

Balozi mpya wa Tanzania nchini Korea Kusini Noel Kaganda alishiriki katika baadhi ya mikutano hiyo iliyofanywa na Rais Mstaafu Dkt. Kikwete na Viongozi hao mbalimbali wa Korea Kusini.

Sambamba na hilo kwa nafasi yake ya Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na kwa kutambua mchango na nafasi yake katika kukuza na kuendeleza sekta ya elimu nchini Tanzania na duniani kote, Chuo Kikuu cha Seoul National University kilimwalika Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete kutoa mhadhara wa wazi katika Chuo hicho.










KATIBU Mkuu wa Wizara ya Afya, Dkt. Grace Magembe, ametembelea banda la TMDA katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) na kupongeza juhudi za Mamlaka katika kudhibiti bidhaa duni na bandia za afya.

Aidha, ameitaka TMDA kuendelea kuimarisha elimu kwa umma kuhusu matumizi salama ya bidhaa za afya ili kulinda afya ya wananchi.

"Tumieni watoa huduma wa ngazi ya Jamii kusaidia kufikisha elimu matumizi salama ya bidhaa za afya kulinda Wananchi.

TMDA mnafanya kazi nzuri na hongereni sana." Amesema Dkt. Grace Magembe.

Mbali na Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, pia TMDA ilipata mgeni Kamishna Jenerali wa Mamlaka ya Kudhibiti na Ku

pambana na Dawa za Kulevya (DCEA), Bw. Aretus Lymo na kuipongeza Mamlaka kwa kazi kubwa ya udhibiti wa bidhaa za afya inayolenga kulinda afya ya wananchi.

Maonesho hayo ya Kimataifa Sabababa yanaendelea hadi Julai 13, 2026.

TMDA ipo kwenye maonesho hayo kutoa elimu kwa Jamii hususani bidhaa duni na bandia na matumizi sahihi ya Dawa.Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya Dkt. Grace Magembe akipokea nakala ya toleo la miaka 20 ya TMDAKatibu Mkuu wa Wizara ya Afya Dkt. Grace Magembe akipata maelezo kuhusu Mahabara inayohamishika (Min kit lab) ambayo ipo katika banda hilo la TMDA ndani ya SabasabaKamishna Jenerali wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA), Bw. Aretus Lymo  (kulia) akipata maelezo kuhusu shughuli za TMDA kutoka kwa Gaudensia Siimwanza Meneja Mawasiliano na Elimu kwa Umma.

 

Na Mwandishi Wetu, Pwani 

MBUNGE Viti Maalum Mkoa wa Pwani Mariam Ibrahim, amechangia Sh. milioni tano kwa ajili ya ujenzi wa Shule Mpya ya Msingi Kisutu iliyopo Jimbo la Bagamoyo mkoani humo. 

Ametoa mchango huo wakati aliposhiriki katika  tukio la upandaji wa miti 300 lililofanyika katika eneo la shule hiyo.
Akizungumza na wananchi, Mbunge Mariam amesema mchango huo ni sehemu ya kuunga mkono juhudi kubwa zinazofanywa na wananchi pamoja na wadau mbalimbali katika kuhakikisha shule hiyo inakamilika. 

Pia amempongeza Mbunge wa Jimbo la Bagamoyo CPA Subira  Mgalu, kwa juhudi zake za kusimamia maendeleo ya elimu na kuendelea kushirikiana na wananchi katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Aidha, amempongeza  Diwani wa Kata ya Kisutu Awesu Muhidini, kwa uongozi wake na namna anavyoshirikiana na wananchi kuipambania shule hiyo hadi kufikia hatua ya sasa.

Mbunge Mariam pia amemshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuwezesha upatikanaji wa eneo lililojengwa shule hiyo, hatua ambayo imefungua fursa ya kuboresha huduma za elimu kwa watoto wa Kata ya Kisutu.

Katika hafla hiyo,amekabidhi sh. milioni 3 papo hapo, huku akiahidi kuwa Sh. milioni mbili zilizobaki atazikabidhi kupitia Mbunge wa Jimbo la Bagamoyo CPA Mgalu, ili kukamilisha ahadi yake ya mchango wa Sh.Milioni 5.










 

Na Mwandishi wetu

Kliniki ya Wateja Maalumu, Wagonjwa wa Kimataifa na Uchunguzi wa Afya wa Kina (Royal, International Patients and Master Health Check-up Clinic) katika Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH) leo imetimiza mwaka mmoja tangu kuanzishwa kwake, huku ikijivunia mafanikio makubwa katika utoaji wa huduma za kibingwa.

Akizungumza katika hafla ya maadhimisho ya mwaka mmoja wa kliniki hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa BMH, Prof. Abel Makubi, amesema kuwa kliniki hiyo ni ya kwanza nchini kutoa huduma za uchunguzi wa afya wa kibingwa kwa mfumo unaowezesha wagonjwa kupata huduma kwa haraka, katika mazingira rafiki na yenye faragha.

Prof. Makubi amesema wateja wa ndani na kutoka nje ya nchi hupata huduma za kibobezi kwa ufanisi, ambapo ndani ya dakika 15 tangu kuwasili wanakuwa wameonana na madaktari bingwa na bobezi.

"Huduma zote muhimu zinapatikana ndani ya kliniki hii, ikiwemo maabara, vipimo mbalimbali, famasi pamoja na malipo, jambo linalopunguza usumbufu kwa wateja na kuongeza ufanisi wa huduma," amesema Prof. Makubi.

Kwa upande wake, Kiongozi wa Kliniki hiyo, Dkt. Saguda Nilla, amesema kuwa katika kipindi cha mwaka mmoja kliniki hiyo imehudumia zaidi ya wateja 28,000, wakiwemo zaidi ya wagonjwa 200 kutoka nje ya Tanzania.

Aidha, amesema zaidi ya watu 300 wamefanya uchunguzi wa afya wa kina (Master Health Check-up) bila kuwa na dalili za ugonjwa, hatua inayowasaidia kufahamu hali zao za afya mapema na kuchukua hatua za kinga.

Baadhi ya wateja wamepongeza ubora wa huduma zinazotolewa katika kliniki hiyo. Bi. Sara Lenday kutoka Iringa amesema alimsafirisha mama yake kwenda BMH kwa matibabu ya moyo, akapata huduma zote kwa haraka na kurejea Iringa siku hiyo hiyo.

Naye Deogratias Haule amesema amekuwa na utamaduni wa kufanya uchunguzi wa afya wa kina kila mwaka licha ya kutokuwa na dalili za ugonjwa.

Ametoa wito kwa Watanzania kujenga utamaduni wa kuchunguza afya zao mara kwa mara, akieleza kuwa hatua hiyo ni muhimu katika kugundua mapema magonjwa yasiyoambukiza na kuongeza nafasi ya matibabu yenye mafanikio.

Ikiwa ni kwa matumizi ya gazeti, tovuti ya habari au taarifa kwa vyombo vya habari, ninaweza pia kuiboresha zaidi kwa mtindo unaoendana na jukwaa husika.









Top News