Na Munir Shemweta, WANMM MTWARA

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Leonard Akwilapoameshuhudia uapisho wa wajumbe wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya na kuwataka wajumbe hao kutenda haki kuacha kutoa maamuzi ya kuwafurahisha watu wakati wa kusikiliza mashauri ya ardhi.

Uapisho huo umeongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Donald Wilson Msengi, na kufanyika leo tarehe 7 Machi 2026 katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa.

Akizungumza mara baada ya kushuhudia uapisho huo, Dkt. Akwilapo aliwaasa wajumbe wa mabaraza hayo kuepuka kutoa maamuzi kwa lengo la kuwafurahisha watu au makundi fulani, badala yake wafanye maamuzi yanayozingatia haki na sheria ili kupunguza migogoro ya ardhi katika jamii.

Alisema wajumbe wanapaswa kutambua kuwa nafasi waliyopewa ni dhamana kubwa kutoka kwa Mungu na Serikali, hivyo wanatakiwa kuitumia kwa uadilifu, uaminifu na kwa kuzingatia misingi ya haki.

“Napenda mtambue kuwa nafasi mlizopewa ni kwa mapenzi ya Mwenyezi Mungu, hivyo mheshimu Mungu kwa kufanya maamuzi yanayoendana na haki na uadilifu,” alisema Dkt. Akwilapo.

Aliongeza kuwa, kazi ya kushughulikia mashauri ya ardhi si rahisi, kwani mara nyingi huwa na pande mbili zinazopingana, lakini wajumbe wanapaswa kufanya maamuzi kwa kuzingatia ushahidi na sheria ili haki ipatikane kwa anayestahili.

“Sina wasiwasi na ninyi, ingawa kazi ni ngumu, lakini mfanye maamuzi kwa kuzingatia haki na siyo kumfurahisha mtu,” alisisitiza.

Dkt. Akwilapo pia alisema uimarishaji wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya ni sehemu ya jitihada za Serikali za kuimarisha mifumo ya utatuzi wa migogoro ya ardhi kwa kusogeza huduma hizo karibu zaidi na wananchi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Mtwara Kanali Msengi aliwapongeza wajumbe hao kwa kuaminiwa kushika nafasi hizo na kuwataka kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia viapo walivyokula na kufanya kazi kwa weledi.

Amesema, wajumbe wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya ni kiungo muhimu katika mfumo wa utatuzi wa migogoro ya ardhi, hivyo wanapaswa kufanya kazi kwa uadilifu ili kujenga imani kwa wananchi.

“Uwepo wa wajumbe wa mabaraza ya ardhi katika wilaya zenu sasa utawezesha wananchi kupata huduma karibu zaidi badala ya kusafiri umbali mrefu kufuata huduma hizo,” alisema.

Ameongeza kuwa, hatua hiyo itasaidia kupunguza gharama na muda ambao wananchi walikuwa wakitumia kufuata huduma za utatuzi wa migogoro ya ardhi katika maeneo ya mbali.

Wajumbe walioapishwa wanatoka katika wilaya za Mtwara, Tandahimba, Newala pamoja na wilaya ya Nanyumbu mkoani Mtwara.

Serikali kupitia Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi imeendelea kuimarisha Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya wilaya ili kuongeza ufanisi katika kusikiliza na kutatua migogoro ya ardhi kwa wakati, jambo litakalosaidia kuimarisha usalama wa milki na kuleta utulivu katika jamii.

Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akizungumza wakati wa kuapishwa kwa wajumbe wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya mkoani Mtwara tarehe 7 Machi 2026.
Mkuu wa Mkoa wa Mtwara Kanali Donald Msengi akimuapisha mmoja wa wajumbe wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya mkoani Mtwara tarehe 7 Machi 2026.
Baadhi ya maofisa wa idara mbalimbali mkoani Mtwara wakiwa katika hafla ya kuapishwa kwa wajumbe wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya mkoani Mtwara tarehe 7 Machi 2026.
Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo (wa pili kushoto mstari wa mbele) na Mkuu wa mkoa wa Mtwara Kanali Donald Msengi(wa tatu kulia mstari wa mbele) pamoja na viongozi wengine wakiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya mkoani Mtwara walioapishwa tarehe 7 Machi 2026. (PICHA ZOTE NA WIZARA YA ARDHI)

Sehemu ya Wajumbe wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya mkoani Mtwara walioapishwa tarehe 7 Machi 2026
Mkuu wa Mkoa wa Mtwara Kanali Donald Msengi akizungumza wakati wa hafla ya kuwaapisha Wajumbe wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya mkoani Mtwara tarehe 7 Machi 2026

JUMLA  ya wanawake 1916 wamefika katika viwanja vya Ofisi za Ardhi kufuatilia hati zao za ardhi na kupata huduma mbalimbali za masuala ya umiliki wa ardhi kupitia programu maalumu ya Samia Ardhi Kliniki inayofanyika Mkoa wa Dodoma.

Wanawake hao wamejitokeza kwa wingi kupata elimu kuhusu haki za umiliki wa ardhi, ushauri wa kitaalamu pamoja na kusaidiwa kukamilisha taratibu za kupata hatimiliki.

Hayo yamesemwa na Kamishna wa Ardhi Msaidizi Mkoa wa Dodoma Bi.Happiness Mtutwa,wakati akifunga kliniki maalum iitwayo Samia Ardhi Kliniki  yenye Kauli Mbiu, Mwanamke; Haki Yako, Miliki Ardhi sasa.

"Katika kliniki hiyo, huduma mbalimbali zimetolewa ambapo hati 694 zimesajiliwa, hati 316 zimekabidhiwa kwa wanawake, migogoro 49 ya ardhi imetatuliwa, na wanawake 105 wamepata ushauri wa kisheria bila malipo. Mpango huo umeonesha mwitikio mkubwa wa wananchi hususan wanawake katika kufuatilia haki zao za umiliki wa ardhi."amesema Bi.Mtutwa

Amesema kuwa Kliniki hiyo imefanyika kuanzia  Machi 2 hadi 7 Machi 2026, ikiwa ni utekelezaji wa maelekezo ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt. Leonard Akwilapo, aliyoyatoa tarehe 12 Februari 2026 jijini Dodoma wakati akihitimisha Kliniki ya Ardhi. Lengo lake ni kuwapa wanawake fursa ya kupata huduma za ardhi kwa urahisi, sambamba na kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani.

Katika kipindi hicho, viongozi wa mkoa wakiongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Rosemary Senyamule pamoja na Mkuu wa Wilaya Mhe. Jabir Shekimweri walitembelea kliniki hiyo kusikiliza na kutatua changamoto mbalimbali za ardhi zinazowakabili wananchi.

Aidha amesema kuwa Taasisi mbalimbali zilishiriki kutoa huduma za ushauri na msaada wa kisheria, zikiwemo Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Chama cha Wanawake Wanasheria Tanzania (TAWLA), Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, pamoja na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu.

Hata hivyo Bi.Mtutwa amesema kuwa Programu ya Samia Ardhi Kliniki imeendelea kuwa jukwaa muhimu la kuwawezesha wanawake kumiliki ardhi kisheria na kupata haki zao, jambo linalochangia maendeleo ya kiuchumi na kijamii kwa familia na jamii kwa ujumla.

Pia amewataka wanawake hao kwenda kuzitumia vizuri hati hizo ili ziweze kuwasaidia kiuchumi kwa kuweza kwenda nazo benki kwa ajili ya kukopa mikopo nafuu itakayowawezesha kuanzisha biashara na kuendelea kuimarisha uchumi wao.

Sambamba na hilo, Bi.Mtutwa pia amekabidhi hati miliki kwa baadhi ya wanawake waliofika katika kliniki hiyo iliyofanyika katika viwanja vya Ofisi ya Kamishna Msaidizi wa Ardhi Mkoa wa Dodoma.

 

Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) Kampasi ya Tanga leo tarehe 7 Machi 2026 kimetekeleza shughuli ya kutoa huduma kwa jamii kwa kutembelea Kituo cha Afya Ngamiani kilichopo jijini Tanga. Katika ziara hiyo, chuo kimetoa msaada wa vifaa tiba pamoja na mahitaji mbalimbali ya msingi kwa watoto waliopo katika wodi ya wazazi.


Sambamba na hilo, watumishi na wanafunzi wa kampasi hiyo wakiongozwa na Mkurugenzi wa Kampasi, Bi. Zawadi Rashidi, walifanya usafi katika maeneo mbalimbali ya kituo hicho ikiwa ni sehemu ya maandalizi kuelekea kilele cha maadhimisho ya miaka 25 ya chuo hicho.

Akizungumza wakati wa kukabidhi misaada hiyo, Bi. Zawadi Rashidi alisema kuwa chuo kina historia na wajibu wa kurudisha kwa jamii inayokizunguka. Alisisitiza kuwa kusaidia jamii ni sehemu ya dhima ya chuo kwa mujibu wa sera zake.

“Msaada huu unaonyesha mapenzi ya dhati kwa jamii inayotuzunguka. Pamoja na wajibu wa kutoa elimu, pia tuna jukumu la kuhudumia jamii inayotuzunguka, hasa katika kipindi hiki ambacho chuo kinasherehekea miaka ishirini na tano tangu kuanzishwa kwake,” alisema.

Aliongeza kuwa msaada uliotolewa unatarajiwa kusaidia kuboresha huduma zinazotolewa katika wodi ya wazazi pamoja na vitengo vingine ndani ya kituo hicho, ambacho kinaendelea kuhudumia wananchi wengi wa jiji la Tanga na maeneo jirani.

Kwa upande wake, Mfamasia wa Kituo cha Afya Ngamiani, Michael Mrosho, aliyepokea misaada hiyo kwa niaba ya Mganga Mfawidhi wa kituo hicho, alishukuru kwa niaba ya uongozi na watumishi wote wa kituo hicho. Alisema msaada huo unaonyesha mapenzi ya dhati ya Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania kwa jamii inayokizunguka.

“Tunawashukuru kwa msaada huu unaoonyesha upendo wenu kwa jamii, hususan wananchi wa Ngamiani. Kupitia vifaa hivi, utoaji wa huduma kwa wagonjwa utaimarika zaidi,” alisema Mrosho.

Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania kinaendelea na mfululizo wa shughuli mbalimbali za kijamii nchini kote kuelekea kilele cha maadhimisho ya miaka 25 tangu kuanzishwa kwake, kwa lengo la kuimarisha uhusiano kati ya chuo na jamii pamoja na kuendeleza utamaduni wa uwajibikaji kwa jamii.




Na WMJJWM – Geita. 

Wanawake wachimbaji madini Mkoani Geita wamehimizwa kutumia fursa za mikopo inayotolewa na Serikali kupitia benki ya NMB ili kukuza na kuinua shughuli zao za uchimbaji na biashara zinazohusiana na sekta ya madini.

Wito huo umetolewa leo Machi 07, 2026, Mkoani humo na Katibu Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dkt. John Jingu wakati akizungumza katika kongamano la wanawake wachimbaji madini lililofanyika mkoani Geita.

Dkt. Jingu amesema Serikali imeweka mazingira rafiki ya kuwawezesha wanawake kiuchumi kupitia mikopo na mafunzo ya ujasiriamali, na kuwataka wanawake wachimbaji madini kujitokeza kuomba mikopo hiyo ili kuimarisha shughuli zao na kuongeza tija katika sekta ya madini.

Amesema wanawake ni uti wa mgongo wa familia, jamii na Taifa, hivyo wanapowezeshwa kiuchumi familia zao hupata maendeleo na ustawi.

“Serikali ipo tayari kusaidia wachimbaji madini, hususan wanawake, ili waweze kunufaika na fursa zilizopo katika sekta ya madini na kuchangia zaidi katika ukuaji wa uchumi,” amesema Dkt. Jingu.

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Chama cha Wanawake Wachimbaji Madini, Salma Ernest amesema chama hicho kimekuwa kikitoa mchango mkubwa katika huduma za kijamii nchini.

salam amesema kupitia chama hicho wamefanikiwa kusaidia miradi mbalimbali ikiwemo ujenzi wa shule mkoani Tanga pamoja na kutoa huduma mbalimbali za kijamii kwa wafungwa katika baadhi ya magereza nchini.

Aidha amesema chama hicho kinaendelea kuwawezesha wanawake wachimbaji madini kwa kuwapa elimu ya fedha, kuwahamasisha kuanzisha miradi ya pamoja na kukuza shughuli zao za kiuchumi ili waweze kujikwamua kiuchumi na kuchangia maendeleo ya jamii.


📌Atoa maelekezo mahsusi kwa Mkandarasi na Wasimamizi wa mradi

Naibu Waziri wa Nishati, Mhe.Salome Makamba leo amekagua utekelezaji wa mradi wa kuzalisha umeme wa Malagarasi (MW 49.5) unaotekelezwa katika Wilaya ya Uvinza mkoani Kigoma ambapo ameeleza kutoridhishwa kwake na kasi ya utekelezaji.

Akiwa katika Kijiji cha Mazungwe wilayani Uvinza Mhe Salome amekagua sehemu mbalimbali za mradi ikiwemo ujenzi wa tuta na uchepushaji mto, ujenzi wa jengo la kuendeshea  mitambo na kambi za wafanyakazi ambapo hakukuta wafanyakazi wa kutosha kama ambavyo mkataba unaelekeza.

Kutokana na hilo, Naibu Waziri wa Nishati amemuagiza mkandarasi kampuni ya Dongfang ya China kuhakikisha kuwa anaongeza wafanyakazi,  vifaa vya kazi na ndani ya mwezi mmoia awe amejenga kambi ya wafanyakazi.

Aidha,  amemtaka Mkandarasi kuwasilisha ratiba mpya  ya utekelezaji wa kazi.

Vilevile, ameagiza wasimamizi wa mradi wa Malagarasi kutoka Kampuni ya Mkandarasi  Mshaurii na TANESCO kuhamia katika eneo la mradi ndani ya mwezi  mmoja ili kuweza kuusimamia mradi huo kwa ukaribu.

"Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ameiagiza Wizara ya Nishati kuzalisha megawati 8000 za umeme ifikapo 2030, hatutakubali mtu atukwamishe katika kufikia malengo haya. Mkandarasi hakikisha unakamilisha kazi ifikapo Oktoba 2027 kama mkataba unavyoelekeza." Amesisitiza Mhe.Salome

Aidha, amemtaka Mkandarasi  Mshauri kampuni ya Multiconsult Norge AS ya Norway na Norplan kutoka Tanzania kuhakikisha kuwa wanamsimamia mkandarasi ipasavyo ili mradi ukamilike kwa wakati na kwa viwango stahiki.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Uvinza, Dinah Mathamani ameeleza kuwa uongozi wa wilaya hiyo utasimamia kwa karibu maelekezo yanayotolewa na Wizara ili mkandarasi atekeleze kazi kulingana na.mkataba.

Naye, Mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati (Umeme na Nishati Jadidifu), Mhandisi Edson Ngabo amesema utekelezaji wa mradi wa Malagarasi kwa saaa ulipaswa kuwa kwenye asilimia 28 ila  umefikia asilimia 23.

Amesema Wizara ya Nishati itaendelea  kumsimamia kwa karibu mkandarasi  ili amalize kazi kwa wakati.

Sehemu nyingne zinazohusisha mradi wa Malagarasi ni upelekaji umeme katika vijiji saba vyenye vitongoji 18 ambapo mradi huo umekamilika kwa asilimia 100.

Pia ujenzi wa njia ya msongo wa kV 132 kutoka eneo la mradi hadi Kidahwe ambao umekamilika kwa asilimia 100.





Mwasisi wa Chama Cha Wanahabari Wanawake Tanzania(TAMWA),Fatma Aloo akizungumza wakati wa Iftari iliyofanyika katika Ofisi za TAMWA jijini Dar es Salkaam kwa kuunganisha Waandishi wa habari wakongwe na wakati na wasasa. Iftaru hiyo imefanyika Machi 06, 2026.


CHAMA cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania, Tanzania Media Women’s Association (TAMWA), kimesisitiza umuhimu wa kuendeleza harakati za kupigania haki za wanawake na watoto huku kikikumbusha historia ya kuanzishwa kwa harakati hizo na mchango wake katika kupambana na dhuluma za kijinsia nchini.

Akizungumza katika Iftari iliyofanyika Machi 06, 2026 ikiwa ni kuelekea maadhimisho ya miaka 37 tangu kuanzishwa kwa TAMWA, mmoja wa waanzilishi wa chama hicho, Fatma Alloo, alisema harakati za kutetea haki za wanawake zilianza muda mrefu na bado zina umuhimu mkubwa hadi leo kutokana na changamoto zinazoendelea kujitokeza.

Alieleza kuwa TAMWA ilianzishwa siku ya maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani, wakati huo ikiwa ni kundi dogo la waandishi wanawake waliokuwa wakifanya kazi kwa karibu na gazeti la Daily News, wakilenga kuibua masuala ya kijinsia katika jamii.

Fatma alisema wakati wanaanzisha harakati hizo walikuwa bado vijana na hawakuwa na uelewa mpana wa aina zote za dhuluma, lakini walikuwa wanashuhudia mateso na changamoto zilizokuwa zikiwakumba wanawake na watoto katika jamii.

Alisisitiza kuwa licha ya jitihada zilizofanyika kwa miaka mingi, dhuluma dhidi ya wanawake bado ipo na hata inaonekana katika baadhi ya nchi zilizoendelea barani Ulaya, jambo linaloonesha kuwa mapambano hayo yanahitaji kuendelea kupewa kipaumbele na vizazi vijavyo.

Pia alisema kwa kusema Wakati wameanza harakati za kuanzisha TAMWA, waume zao walikuwa wakituwaunga mkono  na hiyo waliwatia nguvu zaidi, ili kuendeleza mapambano ya dhuluma kwa wanawake  na watoto.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa TAMWA, Dkt. Rose Reuben, alisema mkutano huo umeandaliwa mahsusi kukusanya na kuhifadhi hadithi na historia ya kazi zilizofanywa na wanachama wa chama hicho katika kutetea haki za binadamu kwa mtazamo wa kijinsia.

Alieleza kuwa pamoja na kukusanya historia, mkutano huo pia unalenga kutambua na kuheshimu mchango wa wanachama waliotoa Kwa muda, nguvu na maarifa yao katika kuimarisha harakati za kupigania haki za wanawake, wakiwemo wale waliotangulia mbele ya haki.

Aidha, TAMWA ilibainisha kuwa katika mafanikio yake, chama hicho kimefanikiwa kupata shamba lenye ukubwa wa takribani hekta 98 ambalo linatarajiwa kusaidia kuendeleza shughuli na miradi ya shirika hilo kwa lengo la kuimarisha mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia.

Chama hicho pia kimeonya kuwa pamoja na uwepo wa sera na sheria mbalimbali za kulinda haki za wanawake na watoto wa kike, bado kuna changamoto kubwa katika utekelezaji wake, hasa kutokana na mabadiliko ya kijamii na kuongezeka kwa vitendo vya ukatili kupitia mitandao ya kijamii.

Kutokana na hali hiyo, TAMWA imevitaka vyombo vya habari, mamlaka za mawasiliano na wadau wengine kushirikiana kikamilifu katika kupambana na ukatili wa kijinsia, hususan unaofanyika mitandaoni, huku jamii ikihimizwa kuacha kuvumilia vitendo hivyo na kulinda watoto dhidi ya mazingira hatarishi.
Tanzania imeungana na Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Nchi za Ukanda wa Bahari ya Hindi (IORA) kuadhimisha miaka 29 ya kuanzishwa kwa jumuiya hiyo katika hafla iliyofanyika katika mji wa Serikali, Mtumba jijini Dodoma ambapo miti ya Matunda na Kivuli imepandwa.

Akiongoza maadhimisho hayo, Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais anayeshughulikia Mazingira Balozi Baraka Luvanda ameshiriki mazoezi mepesi na upandaji miti ya matunda na kivuli uliofanyika katika Ofisi za Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ikiwa ni ishara ya utunzaji wa mazingira na kuimarisha afya za washiriki.

Akizungumza katika maadhimisho hayo, Balozi Luvanda ameeleza namna nchi inavyonufaika na IORA kupitia Jitihada za pamoja za kuhakikisha rasilimali za Bahari ya Hindi zinatumika kwa maendeleo endelevu na kuongeza kuwa Jumuiya hiyo inawawezesha nchi wanachama kukusanya nguvu na kukabiliana na changamoto mbalimbali kwa pamoja.

Pia ameeleza kuwa kupitia jumuiya hiyo nchi wanachama zimekuwa zikipambana na uvuvi haramu, kutangaza fursa zinazopatikana katika bahari ya Hindi hususani uchumi wa buluu, kubadilishana uzoefu na kujengeana uwezo kwa watalaam wa nchi wananchama na kutoa wito kwa wadau kuendelea kushiriki kikamilifu katika shughuli za IORA na kuchangamkia fursa mbalimbali zinazopatikana ndani ya Jumuiya hiyo.

Ameeleza kuwa zoezi la upandaji miti lililofanyika linaunga mkono maono ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kupitia kampeni ya “27 ya Kijani”.

“Hii pia ni sehemu ya utekelezaji wa Sera ya Mambo ya Nje ya mwaka 2001 (Toleo la 2024) na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, ambazo kwa pamoja zinatilia mkazo uhifadhi wa mazingira na ustahimilivu dhidi ya changamoto za kiikolojia,” alisisitiza Balozi Luvanda.

Maadhimisho hayo yamefanyika chini ya kauli mbiu isemayo “IORA INABORESHA MAISHA” (IORA Improves Lives), ikilenga kuongeza uelewa wa umma kuhusu umuhimu wa Jumuiya hiyo kwa jamii za nchi wanachama.








VICTOR MASANGU,KIBAHA

Wafanyakazi wanawake wa kampuni ya SF group ya Jijini Dar es Salaam katika kuadhimisha maadhimisho ya siku ya mwananke duniani wameamua kutoa msaada wa vitu mbali mbali katika shule ya Sekondari Koka pamoja na kufanya matendo ya huruma katika vituo viwili vya kulelea watoto yatima vilivyopo Katika Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha.

Katika kuona umuhimu wa siku hiyo wanawake hao wa kampuni ya SF group katika kukuza sekta ya elimu wameweza kutembelewa wanafunzi wanaosoma katika shule ya Koka sekondari iliyopo katika kata ya Sofu na kutoa msaada wa vitu mbali mbali ikiwemo kompyuta tatu, madaftari, pamoja na taulo za kike ambazo zitakuwa ni mkombozi mkubwa kwa wanafunzi wa kike.

Akizungumza katika sherhe za maadhimisho hayo ambayo yamefanyika katika Jimbo la Kibaha mjini Mkurugenzi wa Rasirimali watu na utawala wa kampuni ya SF Group Marygoreth Faustine ambaye aliongoza na kundi la wanawake kutoka makampuni mbali mbali yaliyopo ndani ya Sf Group amesema kwamba dhamira yao kubwa ni kurudisha fadhila kwa jamii ikiwa sambamba na kusaidia kuinua sekta ya elimu na afya.

"Sisi kama wanawake wa SF Group tumeamua kuitumia siku hii ya kipekee ya maadhimisho ya mwananke duniania kwenda kutembelea baadhi ya maeneo yaliyopo katika Jimbo la Kibha mjini na kwamba tumetoa msaada wa vitu mbali mbali katika shule ya Koka sekondari ikiwemo Kompyuta tatu, taulo za kike, pamoja na madaftari na mahitaji mengine ya msingi ambayo yataweza kuwasaidia wanafunzi katika kuongeza kiwango cha ufaulu," amesema Mariagoreth.

Pia Mkurugenzi huyo amebainisha kwamba katika ziara hiyo wameweza kupata fursa ya kutembelea Zahanati ya Mwendapole na kutoa msaada wa mahitaji mbali mbali katika wodi ya wakinamama na kuwakabidhi msaada wa vifaaa mbali mbali ambayo vitawasaidia wakinamama wajawazito pamoja na wale ambao tayari wameshajifungua.

“Tumeungana kwa pamoja na wanawake wote wa kampuni ya SF Group katika kusherekea maadhimisho ya kilele cha siku ya wanawake duniani kwa kimsingi tumeweza kupata fursa ya kutembelea katika maeneo manne ambapo pia tumefanya matendo ya huruma katika vituo vya watoto yatima," amebainisha Mkurugenzi Mariagoleth.

Pamoja na hayo walikwenda kutembelea kituo cha watoto yatima cha Fadhila kilichopo kata ya misugusugu pamoja na kituo kingine cha Shalom kilichopo kata ya Msangani na kufanya matendo ya huruma na kutoa msaada wa mahitaji mbali mbali ikiwemo sabuni, sukari, unga, mafuta, sabuni za kufulia na kuogea, dawa za meno pamoja na vitu vingine vya msingi ambavyo vitaweza kuwasaidia wattoto hao.

Katika hatua Mkurugenzi huyo amebainisha kwamba lengo kubwa la kwenda kutoa msaada katika maeneo mbali mbali ya Jimbo la Kibaha mjini ni kwa ajili kuonyesha ushirikiano wa pamoja kati yao na jamii amabayo inawazunguka ikiwa pamoja na kuunga mkono juhudi za serikali katika kuleta chachu ya maendeleo na kuisaidia jamii katika mambo mbali mbali ikiwemo afya, elimu, pamoja na huduma za kijamii.

Naye mwalimu mkuu wa shule ya Koka Sekondari Magreth William aliwashukuru kwa dhati wanawake hao wa kampuni ya SF Group kwa msaada huo ambao wameutoa pamoja na kumshukuru kwa dhati Mbunge wa Jimbo la Kibaha mjini Silvestry Koka kwa kutoa sapoti kubwa katika kuboresha sekta ya elimu katika maeneo mbali mbali ikiwemo shule hiyo ya Koka sekondari.

Nao baadhi ya watoto yatima na wanaoishi katika mazingira magumu katika vituo vya Fadhila na Shalom wametoa shukrani zao za dhati kwa wanawake wa kampuni hiyo ya SF Group kwa msaada huo kutoka kwa wanawake wa SF Group.

Wanawake wa kampuni ya SF Group wametumia kilele cha maadhimisho ya siku ya mwanamke duniani kufanya matendo ya Huruma katika sehemu nne ikiwemo kituo cha watoto yatima cha Fadhila, Shalom, zahanati ya Mwendapole pamoja na kutoa msaada katika shule ya Koka sekondari.





















Top News