KAMPUNI ya ALAF, imezindua Kundi la tano la Mpango wa Wanawake katika Uongozi kama sehemu ya maadhimisho ya siku ya Kimataifa ya Wanawake, ambayo huadhimishwa Machi 8 kila mwaka duniani kote.

Uzinduzi huo, uliofanyika jijini Dar es Salaam uliongozwa na kaulimbiu ya ‘Toa Upate’ambapo mgeni rasmi alikuwa ni Katibu Tawala Msaidi wa Mkoa wa Dar es Salaam-Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Zubeda Masoud ambapo ulikwenda sambamba na wafanyakazi kutambua mafanikio ya wanawake, huku wakionyesha dhamira yao ya uongozi, uwezeshaji na kuisaidia jamii.

Akizungumza katika uzinduzi huo Zubeda aliupongeza uongozi wa ALAF kwa kuwapa wanawake umuhimu unaostahili na kuhakikisha wanashika nafasi za juu za uongozi katika kampuni hiyo ikiwa ni pamoja na kushiriki nao katika Siku ya Wanawake.

“Makampuni mengine yanatakiwa kuiga mfano huu wa ALAF kwani huu ni muendelezo mzuri wa kuadhimisha siku ya wanawake duniani,” alisema huku akiipongeza kampuni hiyo pia kwa kuwakumbuka watoto wenye mahitaji maalumu ambao walikabidhiwa viti 10 vyenye magurudumu.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa ALAF, Bibhu Nanda, aliyewakilishwa na Mkuu wa Kitengo cha Mauzo, Sateesh Yamsani, alisema kampuni itaendelea kuunga mkono mipango ya wanawake katika uongozi ili kuhakikisha wanawake wengi zaidi wanapata nafasi za uongozi katika kampuni hiyo.

"Huu unakuwa mpango endelevu ili ALAF iendelee kishika nafasi ya juu katika sekta ya Viwanda kama mwajiri Bora.. tumeona matunda ya mpango huu ulioanza miaka minne iliyopita na kama kampuni tutahakikisha kwamba unakuwa endelevu ili wanawake wengi zaidi waweze kushika nafasi hizi muhimu,”alisisitiza.

Naye Meneja Rasilimali Watu Msaidizi, Rehema Amry alisema: “Huu ni mpango unaolenga kuimarisha uwezo wa uongozi na kusaidia ukuaji wa kitaaluma wa wanawake ndani ya kampuni.”

Alisema maadhimisho ya mwaka huu yana umuhimu wa kipekee kwani ALAF inaadhimisha miaka 65 ya ubora, ubunifu na mchango katika maendeleo ya viwanda Tanzania. “Katika miongo sita iliyopita, kampuni imeendelea kukuza ukuaji jumuishi na kutoa fursa kwa watu wake na jamii inayowahudumia,” aliongeza.

Kwa mujibu wa Rehema, ALAF inapoendelea na safari yake ya ukuaji na matokeo yake chanya kwa jamii, inathibitisha dhamira yake ya kujenga mahali pa kazi shirikishi, ambapo wanawake wanawezeshwa kuongoza, kuhamasisha na kuchangia katika maisha bora ya baadaye.

“ALAF, tunaamini kwamba kuwawezesha wanawake na kuzisaidia jamii zetu kunakwenda sambamba hivyo tunaposherehekea miaka 65 ya ubora, tunaendelea kujitolea kutengeneza fursa kwa wanawake kuongoza, huku tukifanya mabadiliko ya muhimu katika jamii kwani hisani huanzia nyumbani.”

Wakati huo huo, katika ari ya kutoa kwa jamii, wafanyakazi wanawake ALAF walichangia kwa hiari kusaidia ajenda ya kampuni ya uwajibikaji kwa jamii. Kwa juhudi zao za pamoja, viti 10 vya magurudumu vilitolewa kwa watoto wenye mahitaji maalumu, huku kiti kimoja cha magurudumu kikikabidhiwa kwa mfanyakazi wa ALAF, na kusisitiza imani kwamba hisani huanzia nyumbani.



Mafunzo ya siku tano kwa Maafisa Elimu kutoka mikoa 26 ya Tanzania Bara yameanza rasmi jijini Arusha, yakilenga kuwajengea uwezo viongozi hao katika utekelezaji wa majukumu yao ya kiutendaji.

Mafunzo hayo yalifunguliwa Machi 8, 2026 na Naibu Katibu Mkuu anayeshughulikia Elimu kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Atupele Mwambene.

Mafunzo hayo yanasimamiwa na Wakala wa Maendeleo ya Uongozi wa Elimu (ADEM) kwa kushirikiana na taasisi ya Shule Bora, yakihusisha wataalamu kutoka ADEM pamoja na vyuo vikuu mbalimbali Tanzania Bara.

Miongoni mwa mada zinazotolewa ni pamoja na uongozi bunifu wa kimkakati katika kutatua migogoro, mbinu za kutafuta rasilimali fedha na matumizi sahihi ya rasilimali nyingine, pamoja na umuhimu wa ushirikishwaji katika kuongoza sekta ya elimu. Mada nyingine zinahusu ujifunzaji na uatamizi katika uongozi wa elimu.

Aidha, washiriki wanapatiwa maarifa kuhusu matumizi sahihi ya akili hisia (Emotional Intelligence) ili waweze kutambua, kuelewa na kusimamia hisia zao pamoja na za wengine, hatua itakayosaidia kupunguza msongo wa mawazo, kuboresha mawasiliano, kuimarisha ushirikiano na kuongeza tija katika usimamizi wa sekta ya elimu.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, Mwambene aliipongeza ADEM na Shule Bora kwa kufanikisha maandalizi ya mafunzo hayo na kuwataka washiriki kuyatumia vyema maarifa watakayopata.

Aliwasisitiza viongozi hao kushughulikia kwa umakini malalamiko yanayojitokeza katika maeneo yao ya kazi pamoja na kutekeleza kwa ufanisi malengo ya kisera na mabadiliko ya mitaala.

“Ninawaomba mhakikishe mnaandaa mazingira rafiki ya kujifunza na kujifunzia, na mnasimamia changamoto zinazotokana na malalamiko katika maeneo mnayoyasimamia,” alisema Mwambene.

Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa ADEM, Dk. Maulid J. Maulid, alisema ushirikiano kati ya taasisi hiyo na Shule Bora umefanikisha uandaaji wa matini mbalimbali za mafunzo kwa viongozi wa elimu.

Alizitaja baadhi ya matini hizo kuwa ni pamoja na za uanzishwaji na usimamizi wa Jumuiya za Kujifunzia, usimamizi wa uongozi wa kujifunza, pamoja na mafunzo kwa viongozi wa elimu katika ngazi za mikoa na wilaya.

Dk. Maulid alisema mafunzo hayo yatawasaidia viongozi wa elimu kuwa na maono ya mageuzi makubwa yanayoendana na mabadiliko ya kiteknolojia pamoja na dira ya maendeleo ya Taifa 2050.

Aliongeza kuwa kupitia mafunzo hayo viongozi hao watafahamu umuhimu wa mipango ya kisekta pamoja na namna sahihi ya kutathmini mafanikio na changamoto zinazojitokeza katika utekelezaji wa majukumu yao.

Mafunzo hayo yanatarajiwa kuhitimishwa Machi 12, 2026 ambapo mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Kamishna wa Elimu, Dk. Lyabwene Mutahabwa.








▪️Ni ya 4 barani Afrika, nyuma ya Botswana, Morocco na Zambia

▪️Alama ya Tanzania yapanda hadi 68.04 mwaka 2025 kutoka 62.75 (2024) na 46.38 (2023)

▪️Tanzania yaorodheshwa nafasi ya 15 duniani kwenye Best Practices Mineral Potential Index kwa alama 75.00

▪️Utafiti uliwahusisha wataalam na viongozi 2,304 wa kampuni za utafiti na uchimbaji.

▪️Rais Samia apongezwa kwa mazingira mazuri ya Uwekezaji Tanzania

Tanzania imeendelea kuimarisha nafasi yake kama kivutio cha kimataifa cha uwekezaji kwenye sekta ya madini baada ya kuorodheshwa miongoni mwa maeneo yanayoongoza barani Afrika, kwa mujibu wa ripoti ya Fraser Institute, Annual Survey of Mining Companies 2025.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo, Tanzania imepata nafasi ya 34 kati ya maeneo 68 duniani yaliyotathminiwa katika Investment Attractiveness Index (IAI), kielezo kinachotumiwa na wawekezaji na kampuni za utafiti wa madini kuamua wapi waelekeze mitaji ya utafiti na maendeleo ya miradi.  

Katika muktadha wa Afrika, Tanzania imeendelea kushika nafasi ya juu kwa kuwa ya 4 barani Afrika katika IAI, ikifuata Botswana, Morocco na Zambia, hatua inayothibitisha ushindani wa Tanzania katika kuvutia mitaji ya kimataifa ya utafiti na uwekezaji wa madini.  

Ripoti inaonesha pia mwenendo chanya wa kupanda kwa alama za Tanzania, ambapo alama ya IAI imefikia 68.04 mwaka 2025, ikilinganishwa na 62.75 mwaka 2024 na 46.38 mwaka 2023 mwenendo unaoashiria kuongezeka kwa uaminifu na mvuto wa Tanzania kwa wawekezaji wa sekta ya madini.  

Kwa maelezo ya ripoti, IAI hujengwa kwa kuzingatia vipengele viwili vikuu vinavyoongoza maamuzi ya uwekezaji: uwezo wa kijiolojia wa rasilimali (mineral potential) na mazingira ya jumla ya kufanya biashara kwenye sekta husika. Ripoti hiyo inaeleza kuwa katika hesabu yake, asilimia 60 ya uzito huenda kwenye mineral potential na asilimia 40 huenda kwenye policy framework, ili kutoa taswira ya mvuto wa eneo husika kwa uwekezaji wa utafiti na uchimbaji.  

Katika kipengele cha Best Practices Mineral Potential Index kinachoangalia mvuto wa kijiolojia kama eneo lingekuwa na kanuni bora zaidi duniani Tanzania imeorodheshwa nafasi ya 15 duniani kwa alama 75.00, jambo linaloonesha kwa uwazi ukubwa wa fursa na uwezo wa rasilimali madini zilizopo nchini.  

Utafiti huu wa Fraser Institute ni miongoni mwa rejea muhimu zinazotumiwa kimataifa na sekta binafsi, taasisi za utafiti na wadau mbalimbali kutathmini mwenendo wa masoko ya uwekezaji wa madini. Kwa mujibu wa taarifa ya utafiti, dodoso lilipelekwa kwa viongozi na wataalam 2,304 wa kampuni za utafiti na uchimbaji, na waliotoa majibu waliripoti matumizi ya pamoja ya takribani Dola za Marekani bilioni 4.2 kwenye shughuli za utafiti wa madini mwaka 2025.  

Kwa Tanzania, nafasi hii inaongeza msukumo kwenye jitihada za Serikali za kuendelea kuimarisha sekta ya madini kama nguzo muhimu ya uchumi ikiwemo kuongeza utafiti, kuvutia mitaji mikubwa ya uendelezaji wa miradi, na kukuza ushiriki wa Watanzania katika mnyororo mzima wa thamani wa madini.  

Wataalamu wa uchumi na wadau wa sekta ya madini nchini wamempongeza Rais Dkt. Samia S. Hassan kwa kuvutia uwekezaji mkubwa kwenye sekta ya madini nchini Tanzania,huku wengi wakibashiri kuwa sekta ya madini kuwa nguzo kuu ya uchumi wa Tanzania kwa miaka michache ijayo.





 

Na Mwandishi wetu Dodoma

Jumuiya ya Wanawake wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA) leo alasiri, tarehe 9 Machi, 2026 wamesambaza bure majiko banifu 300 kwa kaya zenye kipato cha chini katika Halmashauri ya wilaya ya Bahi mkoani Dodoma ambapo zoezi hilo liliongozwa na Mkuu wa wilaya hiyo, Mhe. Joachim Nyingo.

Akizungumza wakati wa zoezi la ugawaji wa majiko hayo banifu 300 yenye thamani ya shilingi milioni 16 ambayo yametolewa wa Wanawake hao kutoka REA; Mhe. Nyingo ametoa wito kwa kaya hizo kuyatunza na kuyatumia kama kichocheo cha kuendelea kutumia bidhaa za nishati safi ya kupikia kama msisitizo wa matumizi ya nishati safi na salama kwa ajili ya kutunza na kuhifadhi mazingira.

“Ongezeko la Watu, vijijini linasababisha ukataji mkubwa miti kwa ajili ya kutengeneza mkaa na kuni ila kwa matumizi ya majiko haya banifu; ninaamini yanasaidia kupunguza matumizi ya kuni na mkaa, lakini pia yataokoa muda wa kuandaa chakula na hapo hapo kutunza mazingira” Amekaririwa Mkuu wa wilaya huyo.

“Niwaombe wanufaika wote, mkayatunze majiko hayo na mkawe mabalozi wa teknolojia za nishati safi. Naomba pia kutoa wito kwa wasambazaji wa teknolojia za nishati safi, endeleeni kusogeza bidhaa za nishati safi ya kupikia hadi huku vijijini.”

“Nawashukuru Wanawake wa REA kwa kuichagua wilaya ya Bahi na kugawa majiko hayo kwa kaya maskini ili kupunguza matumizi ya kuni na mkaa”. Amesema, Mhe. Joachim Nyingo.

Naye Mwakilishi wa Mkurugenzi Mkuu kutoka REA; Dkt. Joseph Sambali ambaye ni Mtaalam wa Nishati na Jinsia amesema, tukio la ugawaji wa majiko banifu bure kwa kaya hizo katika Kata tatu za Bahi; Mpamantwa na Ibihwa ni juhudi za utekelezaji wa Mkakati wa Kifaifa wa Nishati Safi ya Kupikia na unalenga hadi ifikapo mwaka 2034 zaidi ya asilimia 80 ya Watanzania wawe wanatumia nishati safi.



 






FARIDA MANGUBE, KILOSA, MOROGORO
HOFU na simanzi vimetanda katika Kijiji cha Changarawe wilayani Kilosa mkoani Morogoro baada ya mwili wa mwanamke aliyeripotiwa kutoweka kwa zaidi ya miezi mitatu kugundulika ukiwa umefukiwa ndani ya nyumba aliyokuwa akiishi na rafiki yake wa kiume, ambaye naye hajulikani alipo.

Mwanamke huyo ametambuliwa kwa jina la Lilian Danstan Manga (27) ambaye aliripotiwa kutoweka tangu Desemba 11, 2025 katika Kitongoji cha Kipera, Kata ya Masanze.

Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, SACP Alex Mkama, mwili huo uligunduliwa baada ya mwanamke aliyekuwa akifanya usafi katika nyumba hiyo kubaini tuta la udongo ndani ya chumba.

“Baada ya taarifa hiyo kupokelewa, uchunguzi ulifanyika na hatimaye mwili wa mwanamke huyo kufukuliwa ndani ya nyumba hiyo,” alisema Mkama

Jeshi la polisi linamtafuta mtuhumuwa wa tukio hilo ambaye inaelezwa alikuwa akiishi na mwanamke huyo.

Baba wa marehemu, Danstan Albano Manga, amesema familia imepata pigo kubwa kufuatia tukio hilo.

Naye Felista Simon, jirani na mkazi wa Changarawe, amesema tukio hilo limewatia hofu wakazi wa eneo hilo.

“Hatukutarajia kabisa tukio la aina hii kutokea katika kijiji chetu,” alisema.

Kwa upande wake Nicholous Mkoma, Mwenyekiti wa Kijiji cha Changarawe, amesema viongozi wa kijiji walichukua hatua za haraka baada ya kupokea taarifa hizo na kushirikiana na vyombo vya usalama kufanikisha uchunguzi.
BENKI ya Maendeleo ya Kilimo (TADB), imesema katika kutambua umuhimu wa kusogeza huduma karibu zaidi kwa wadau wake inaendelea na mipango ya kufungua ofisi rasmi ya TADB Zanzibar.

Benki hiyo imesema kwa sasa inatoa huduma zake kwa ngazi ya kanda visiwani Zanzibar kwenye ofisi zilizopo Jengo la ZURA Mtaa wa Maisara.

Ahadi hiyo ilitolewa jana Unguja na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki hiyo, Frank Nyabundege, wakati wa futari na wadau wa Zanzibar ambayo pia ilihudhuriwa na Dk Juma Malik Akili ambaye ni Waziri wa Fedha na Mipango wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ambaye alimwakilisha Mhe.Rais wa Zanzibar, Waziri wa Kilimo, Suleiman Masoud Makame, Waziri wa Nchi ofisi ya Makam wa Pili wa Rais, Sera, Uratibu na Baraza la Wawakilishi Mhe. Hamza Hassan Juma, na Waziri wa Uchumi wa buluu, Masoud Ali.

Alisema hatua ya kufungua ofisi rasmi visiwani Zanzibar itasaidia kuongeza upatikanaji wa huduma za kifedha na ushauri wa kitaalamu kwa wakulima, wafugaji na wavuvi katika kanda ya Zanzibar.

Alisema tangu kuanzishwa kwake, benki ya TADB imeweza kutoa huduma jumuishi za kifedha kwa kutoa mikopo Jumla shilingi bilioni 12.47 kwa Zanzibar, ikijumuisha Unguja na Pemba,

Alsiema Benki imeweza kuchagiza uwekezaji katika miradi 49 katika maeneo makuu ya uwekezaji yalikuwa usindikaji wa mazao ya kilimo (milioni 208), maghala ya kutunza baridi (milioni 4.5).

Alisema ununuzi wa mazao kutoka kwa wazalishaji shilingi bilioni 6.65), umwagiliaji (milioni 175), matumizi ya mitambo ya kilimo (milioni 153), pembejeo za kilimo (bilioni 1.6), mifugo hai (bilioni 1.14) na mikopo kwa wanawake na vijana (bilioni 1.07) na ufadhili wa mali kama vile malori, mabanda na vizimba vya wanyama (bilioni 1.94).

Alisema Benki imewezesha utendaji wa minyororo ya thamani iliyofanya vizuri zaidi ilikuwa karafuu (bilioni 6.54), kuku (bilioni 3.58), na maziwa (bilioni 1.17) na kutaja minyororo mingine ya thamani kuwa ni (mahindi, mpunga, matunda na mboga) ilipokea jumla ya (milioni 420).

Nyabundege alisema TADB imeweza kuwakifia jumla ya wanufaika 571, kati yao wanawake walikuwa 221, wanaume 350, na kati ya wanufaika 571 vijana ni165.

“Mbali na shughuli za utoaji wa mikopo, Benki pia inatambua umuhimu wa kutekeleza wajibu wake kwa jamii kupitia dhana ya uwajibikaji wa kijamii wa taasisi (Corporate Social Responsibility). Katika tukio hili la leo, Benki imeandaa misaada mbalimbali inayotolewa kwa baadhi ya makundi maalum katika jamii,” alisema.

Aidha, alisema misaada hiyo inahusisha pembejeo za kilimo, misaada wa kifedha pamoja na vyakula, iliyolenga kuwasaidia watu wenye mahitaji.

“ Naomba kukujulisha kuwa katika majitoleo yetu Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) tumeweza kukabidhi Misaada mbalimbalj kwa vituo viwili vya watoto wenye mahitaji maalumu hapa Zanzibar,” alisema.

Aidha, alisema Benki imepanga kuchagiza shughuli za Vikundi vya Vijana, Wanawake Pamoja na wanaume kuwawezesha ili kukuza ufugaji na kilimo hapa Zanzibar.

Aliishukuru Serikali kwa kuendelea kuweka mazingira wezeshi yanayowezesha taasisi kama Benki hiyo kuendelea kuwahudumia wakulima, wafugaji na wavuvi nchini.

“Sera na mipango ya Serikali imeendelea kutoa msukumo mkubwa katika kukuza sekta ya kilimo ambayo ni mhimili muhimu wa uchumi wa Taifa letu,” alisema.

“Tunapenda kuendelea kushirikiana kwa karibu na Serikali pamoja na wadau wengine katika kuhakikisha kuwa sekta ya kilimo, ufugaji na uvuvi inaendelea kukua na kuchangia zaidi katika maendeleo ya uchumi na ustawi wa wananchi wetu,” alisema na kuongeza.

“ Tunawashukuru sana kwa kuitikia mwaliko wetu na kuja kushirikiana nasi katika tukio hili la kuimarisha uhusiano na ushirikiano wetu,” alisema Nyabundege









Na FARIDA MANGUBE, MOROGORO

Wanawake wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Morogoro wameungana na wanawake wengine kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani inayoadhimishwa kila ifikapo Machi 8 kila mwaka huku wakisisitiza umuhimu wa wanawake kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya jamii na taifa.

Kwa Mkoa wa Morogoro maadhimisho hayo yamefanyika katika viwanja vya Shule ya Msingi Fulwe, Halmashauri ya Wilaya ya Morogoro, ambapo wanawake wa TRA Mkoa wa Morogoro walishiriki pamoja na wanawake kutoka taasisi na makundi mbalimbali kuadhimisha siku hiyo maalum inayotambua mchango wa wanawake katika nyanja mbalimbali za maendeleo.

Akizungumza wakati wa maadhimisho hayo Meneja Msaidizi Ukaguzi TRA Mkoa wa Morogoro Bi Beatrice Steven amesema kuwa ushiriki wao katika siku hiyo unaonesha dhamira ya taasisi hiyo kuendelea kuunga mkono juhudi za kuwawezesha wanawake na kuhamasisha usawa wa kijinsia katika jamii.

Amesema wanawake wana nafasi kubwa katika kuchangia maendeleo ya kiuchumi ya taifa kupitia majukumu yao mbalimbali ikiwemo katika sekta ya ukusanyaji wa mapato, biashara, elimu na uongozi, hivyo ni muhimu kuendelea kuhamasisha ushiriki wao katika maendeleo.

Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani ni fursa ya kuimarisha mshikamano, kubadilishana uzoefu na kujadili changamoto zinazowakabili wanawake ili kutafuta suluhisho litakalowezesha maendeleo yao na ya jamii kwa ujumla.

Maadhimisho hayo yalipambwa na shughuli mbalimbali zikiwemo maandamano ya amani, burudani pamoja na utoaji wa ujumbe unaohamasisha jamii kuendelea kuthamini mchango wa wanawake katika maendeleo ya taifa.

Siku ya Wanawake Duniani huadhimishwa kila mwaka Machi 8 duniani kote kwa lengo la kutambua mafanikio ya wanawake katika nyanja za kijamii, kiuchumi na kisiasa pamoja na kuendelea kuhamasisha usawa wa kijinsia.






Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dkt. Asha-Rose Migiro, leo Jumatatu,Machi 9,2026, amefungua rasmi mafunzo maalum ya Uongozi na Utawala Bora kwa viongozi na watendaji waandamizi wa Chama yanayofanyika katika Ukumbi wa Mount Royal, Mkoani Iringa.

Mafunzo hayo ya siku nne yameandaliwa na Jitegemee Holdings Company Limited (JHCL) kwa kushirikiana na Taasisi ya Wakurugenzi Tanzania (IoDT), na yanawaleta pamoja wajumbe wa Bodi, Menejimenti ya Jitegemee Holdings pamoja na viongozi waandamizi wa CCM.

Akifungua mafunzo hayo, Dkt. Migiro amesema kuwa uongozi na utawala bora ni msingi muhimu wa kuimarisha taasisi na kuendeleza maendeleo ya Taifa, akisisitiza kuwa mafunzo hayo yanaendana na utekelezaji wa Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu wa 2025 pamoja na maono ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Aidha, amewataka washiriki kutumia fursa ya mafunzo hayo kujenga uwezo wa kiuongozi na kuhakikisha maarifa watakayopata yanatumika kuimarisha utendaji wa taasisi wanazoziongoza.










Top News