Afisa Tawala wa Wilaya ya Morogoro, Bi. Janeth Chatta,akizungumza wakati akifunga mafunzo ya wasimamizi wa shughuli za ghala kwa msimu wa biashara wa mbaazi na dengu 2026/2027 yaliyofanyika wilayani humo kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya ya Morogoro.

Kaimu Mkurugenzi wa Uratibu na Ubora wa WRRB, Bw. Mwita Thomas,akizungumza wakati wa ufungaji mafunzo ya wasimamizi wa shughuli za ghala kwa msimu wa biashara wa mbaazi na dengu 2026/2027 yaliyofanyika Morogoro.

Sehemu ya washiriki wakimsikiliza Afisa Tawala wa Wilaya ya Morogoro, Bi. Janeth Chatta (hayupo pichani) wakati akifunga mafunzo ya wasimamizi wa shughuli za ghala kwa msimu wa biashara wa mbaazi na dengu 2026/2027 yaliyofanyika wilayani humo kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya ya Morogoro.

Afisa Tawala wa Wilaya ya Morogoro, Bi. Janeth Chatta akiwa katika picha ya pamoja na washiriki mara baada ya kufunga  mafunzo ya wasimamizi wa shughuli za ghala kwa msimu wa biashara wa mbaazi na dengu 2026/2027 yaliyofanyika wilayani humo kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya ya Morogoro.

Na.Mwandishi Wetu-MOROGORO

Watumishi na wasimamizi wa shughuli za ghala nchini wametakiwa kutekeleza majukumu yao kwa uadilifu, weledi na uwajibikaji ili kuimarisha Mfumo wa Stakabadhi za Ghala na kuongeza ufanisi katika biashara ya mazao ya kilimo.

Wito huo umetolewa na Afisa Tawala wa Wilaya ya Morogoro, Bi. Janeth Chatta, kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya ya Morogoro, alipokuwa akifunga mafunzo ya wasimamizi wa shughuli za ghala kwa msimu wa biashara wa mbaazi na dengu 2026/2027 yaliyofanyika wilayani humo.

Bi. Chatta amesema uadilifu wa watendaji wa mfumo ni msingi wa kujenga imani kwa wakulima, wanunuzi na taasisi za fedha, huku akisisitiza kuwa Mfumo huo umeendelea kuwa nyenzo muhimu ya kuhakikisha biashara ya mazao inafanyika kwa uwazi, ubora na ushindani.

Amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan inaendelea kuhimiza matumizi ya Mfumo huo pamoja na Soko la Bidhaa Tanzania (TMX) ili kuongeza thamani ya mazao, kupanua fursa za masoko yenye ushindani na kuongeza manufaa kwa wakulima.

Aidha, amewataka washiriki kutumia maarifa waliyoyapata kutekeleza majukumu yao kwa weledi, kuendana na mabadiliko ya teknolojia na kuhakikisha taarifa za mazao zinakuwa sahihi na kwa wakati.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Uratibu na Ubora wa WRRB, Bw. Mwita Thomas, amewataka wahitimu wa mafunzo hayo kuzingatia sheria, kanuni na taratibu walizofundishwa ili kutekeleza majukumu yao kwa uadilifu, weledi na uwajibikaji, pamoja na kulinda hadhi ya Mfumo wa Stakabadhi za Ghala.

Mafunzo hayo yaliyoandaliwa na WRRB yamefanyika kwa siku tano na yamehudhuriwa na washiriki 103 kutoka kampuni za uendeshaji wa ghala na wadau mbalimbali wa Mfumo huo.

 

Wafugaji nchini wanatarajiwa kunufaika na biashara ya kisasa ya mifugo baada ya Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) kuanza kuingiza mifugo katika Mfumo wa Stakabadhi za Ghala, utakaounganisha taarifa za mifugo kidijitali na kuwawezesha wanunuzi kushindana kwa uwazi kupitia Soko la Bidhaa Tanzania (TMX).

Akizungumza katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), Mkurugenzi Mtendaji wa WRRB, Bw. Asangye Bangu, amesema baada ya mafanikio ya kusimamia bidhaa 18 za mazao ya kilimo kupitia mfumo huo, sasa bodi imepanua huduma zake kwa kujumuisha mifugo.

Amesema hatua hiyo inatokana na mahitaji ya wafugaji waliokuwa wakihoji kwa nini mfumo huo unawanufaisha wakulima pekee huku sekta ya mifugo ikibaki nje.

"Tumekuja na bidhaa mpya ambazo zimeongezwa kwenye mfumo, na kubwa zaidi tumewafikia wafugaji. Tulikuwa tunasimamia bidhaa 18 za mazao ya kilimo, lakini sasa tumeingia rasmi kwenye bidhaa za mifugo," amesema.

Bw. Bangu amesema WRRB inalenga kuunganisha biashara ya mifugo na TMX, ambapo taarifa za kila mnyama zitawekwa kidijitali ili wanunuzi waweze kuzifikia kwa urahisi, kushindana kwa uwazi na kufanya maamuzi ya ununuzi kwa kutumia taarifa sahihi badala ya makadirio.

Ameeleza kuwa mfumo huo utatumia taarifa zinazopatikana kupitia hereni za utambuzi wa mifugo zilizozinduliwa na Rais Samia Suluhu Hassan, ambazo zina namba maalumu zinazobeba taarifa za kila mnyama.

"Tunafahamu Mheshimiwa Rais Samia miaka miwili iliyopita alizindua uwekaji wa hereni kwenye mifugo. Sisi kama WRRB tunapiga hatua zaidi kwa kutumia taarifa zilizopo kwenye hereni hizo kuingiza mifugo kwenye Mfumo wa Stakabadhi za Ghala. Hereni hiyo ndiyo itakuwa msingi wa stakabadhi kwa kuwa ina namba na taarifa zote za mnyama," amesema.

Amefafanua kuwa mfumo huo utawanufaisha wafugaji wanaojishughulisha na unenepeshaji wa mifugo kwa kuwa mifugo yao itahifadhiwa katika maeneo maalumu yatakayokuwa yanatambulika kama ghala, huku wafugaji wakipewa stakabadhi zitakazowawezesha kupata mikopo kutoka taasisi za fedha.

Kwa mujibu wa Bangu, WRRB tayari imefikia makubaliano na Benki ya NBC ambayo imekubali kutoa mikopo kwa wafugaji watakaoweka mifugo yao kwenye ghala.

"Wengi wanauliza ghala litakuwaje. Kwa upande wa mifugo, zizi ndilo litakuwa ghala. Mifugo itatunzwa katika maeneo maalumu yenye chakula na huduma za matibabu, huku mfugaji akiwa na stakabadhi inayomwezesha kupata fedha bila kulazimika kuuza mifugo yake mapema," amesema.

Bangu amesema hatua nyingine muhimu ni kuondoa utaratibu wa kupanga bei kwa kutazama mwonekano wa mnyama pekee, badala yake mifugo itapimwa kwa uzito ili bei iweze kuamuliwa kwa kuzingatia kilo halisi za mnyama.

"Leo hii kwenye minada mingi ng'ombe anapimwa kwa macho, anaonekana mnene au mwembamba ndipo bei inawekwa. Sisi tunataka mifugo ipimwe kwa uzito ili bei iwe ya haki kwa mfugaji na mnunuzi. Hii itakuwa mkombozi mkubwa kwa wafugaji na pia itarahisisha upatikanaji wa taarifa zinazohitajika katika masoko ya ndani na kimataifa," amesema.

 

Serikali imewaagiza wazalishaji wote nchini kutumia alama ya 'Made in Tanzania' ili kuongeza imani kwa bidhaa zinazozalishwa nchini na kuimarisha ushindani wake katika masoko ya kimataifa.

Agizo hilo limetolewa  na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Immanuel Nchimbi, kwenye kilele cha Usiku wa Jubilei ya Dhahabu (Miaka 50) ya Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TANTRADE), uliofanyika Ukumbi wa Mlimani City, Dar es Salaam. Sherehe hizo zilienda sambamba na utoaji wa tuzo kwa washirika muhimu wa mamlaka hiyo. Udhibiti wa Viwango na Huduma za Kifedha.

Aidha, Makamu wa Rais amezitaka taasisi zinazosimamia viwango na huduma za kifedha kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi ili kuhakikisha bidhaa za Tanzania zinakidhi viwango vya kimataifa. Alisema matumizi ya alama ya 'Made in Tanzania' yataongeza utambulisho wa bidhaa zenye ubora na kuimarisha heshima ya taifa katika biashara za kimataifa.

 "Nazipongeza taasisi za fedha kwa kutoa mikopo yenye masharti nafuu kwa viwanda vidogo na vya kati, akisema hatua hiyo imeendelea kupunguza changamoto za upatikanaji wa mitaji kwa wajasiriamali na kuchochea ukuaji wa uzalishaji nchini."amesema Balozi Nchimbi

Amesema Serikali itaendelea kuweka sera rafiki, kuboresha miundombinu na kuimarisha sekta binafsi ili kujenga uchumi wa viwanda wenye ushindani. Ameongeza kuwa maadhimisho ya Jubilei ya Dhahabu ya TANTRADE ni fursa ya kutathmini mafanikio yaliyopatikana, ikiwemo kuongezeka kwa viwanda, uzalishaji, ajira na upanuzi wa masoko ya bidhaa za Tanzania duniani.

Kwa upande wake Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Judith Kapinga (Mb), amesisitiza kuwa manufaa makubwa ya rasilimali zilizopo nchini yatapatikana Tanzania itakapowekeza katika kuchakata na kuzalisha bidhaa za mwisho zenye ubora wa juu badala ya kuuza malighafi ghafi nje ya nchi.

Waziri Kapinga amebainisha kuwa hatua hiyo itafungua masoko mapya, itaongeza thamani ya mauzo ya nje, na kuinua uchumi wa wananchi kwa ujumla.

Mhe. Kapinga ameeleza kuwa, ili kujenga uchumi imara wa viwanda na wenye ushindani, kuna haja ya kubadili mtazamo wa kibiashara kwa kuhakikisha mazao ya kilimo, mifugo, uvuvi, misitu na madini yanageuzwa kuwa bidhaa zilizofungashwa vizuri na kukidhi viwango vya kimataifa.

Amesisitiza kuwa uwekezaji mkubwa katika teknolojia za kisasa una mchango mkubwa katika kuongeza kiwango cha uzalishaji, kuboresha ubora wa bidhaa zinazotengenezwa nchini, kupunguza gharama za uendeshaji, na kuzipa bidhaa za Tanzania uwezo mkubwa wa kushindana katika soko la kimataifa.

Munir Shemweta, Misungwi

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Dkt. Leonard Akwilapo amewatahadharisha viongozi wa vijiji nchini kuacha kujihusisha moja kwa moja na uuzaji wa ardhi bila kufuata taratibu za kisheria, akisema tabia hiyo imekuwa chanzo kikubwa cha migogoro ya ardhi katika maeneo mbalimbali nchini.

Dkt. Akwilapo ametoa onyo hilo Julai 6, 2026 wilayani Misungwi mkoani Mwanza wakati wa hafla ya kukabidhi hati 668 za hakimiliki za kimila kwa wananchi wa vijiji vya Ndinga na Lubuga. Alisisitiza kuwa viongozi wa vijiji, wakiwemo wenyeviti, ni wasimamizi wa ardhi na si wauzaji, hivyo maamuzi ya kuuza ardhi ya kijiji yanapaswa kufanywa kwa kufuata sheria kupitia mikutano ya vijiji na kupata ridhaa ya halmashauri husika.

"Mnapotaka kuuza ardhi kwa watu lazima kijiji kupitia mikutano ya kijiji na halmashauri kikubaliane na hilo. Asije akawa mwenyekiti anaingia kwenye makubaliano peke yake. Tunapiga vita suala hilo kwa sababu limetuingiza kwenye matatizo mengi katika maeneo mbalimbali," alisema Dkt. Akwilapo, akibainisha kuwa kauli hiyo inawahusu viongozi wa vijiji kote nchini na si Misungwi pekee.

Waziri huyo pia alisisitiza kuwa Serikali haitavumilia ubaguzi wa aina yoyote katika umiliki wa ardhi, ikiwemo ubaguzi wa kijinsia, kikabila au kwa misingi mingine. Alieleza kuwa sera na sheria za ardhi zinatambua haki sawa kwa wananchi wote kumiliki ardhi, huku wataalamu wa sekta hiyo wakitakiwa kuendelea kuzisimamia ipasavyo ili kuhakikisha haki inatendeka kwa kila Mtanzania.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Misungwi, Bi. Johari Simizi alisema wilaya hiyo kwa sasa ndiyo eneo linalopokea kasi kubwa ya ukuaji wa makazi kutoka maeneo mengine ya Mkoa wa Mwanza, hali inayohitaji upangaji bora wa matumizi ya ardhi.

Alisema wananchi wa Misungwi wanahitaji mji uliopangwa vizuri kupitia umilikishwaji rasmi wa ardhi ili kuondoa makazi holela na kuifanya wilaya hiyo kuwa na mwonekano unaovutia.

Naye Mbunge wa Jimbo la Misungwi, Mhe. Silvery Salvatory aliitaka Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kuongeza elimu kwa wananchi kuhusu matumizi na umuhimu wa nyaraka za umiliki wa ardhi, akisema baadhi ya wanufaika wa hati bado hawana uelewa wa kutosha kuhusu haki na wajibu unaoambatana na nyaraka hizo.

Akizungumza katika hafla hiyo, Kamishna wa Ardhi Msaidizi Mkoa wa Mwanza, Bw. Wilson Luge aliwapongeza wananchi wa Misungwi kwa mwitikio mkubwa wa kushiriki zoezi la urasimishaji wa ardhi, akisema hatua hiyo imeifanya wilaya hiyo kuwa mfano wa kuigwa na maeneo mengine katika juhudi za kupunguza migogoro ya ardhi kupitia upimaji na utoaji wa hati za umiliki.

Kwa niaba ya wanufaika, Bw. Shije Mashaka aliishukuru Serikali kwa kuwawezesha wananchi kumiliki ardhi kwa hati za hakimiliki za kimila, akieleza kuwa hatua hiyo itasaidia kuondoa migogoro ya mipaka iliyokuwa ikiwasumbua kwa muda mrefu.

Katika utekelezaji wa mradi wa upangaji na upimaji ardhi, Halmashauri ya Wilaya ya Misungwi mkoa wa Mwanza iliipa kampuni ya GMS Geo Tech Consultancy Co. Ltd kazi ya kupima vijiji vya Ndinga na Lubuga, ambapo jumla ya hati 668 zilitolewa kwa wananchi katika awamu ya kwanza ya mradi huo.


Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makakazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akiakabidhi hati za Hakimiliki za Kimila kwa wananchi wa Misungwi mkoani Mwanza wakati wa hafla ya kukabidhi hati hizo iliyofanyika wilayani humo Julai 6, 2026. Kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Misungwi Bi. 
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makakazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akiwa katika picha ya Pamoja na wananchi wa wilaya ya Misungwi mara baada ya kuwakabidhi Hati za Hakimiliki za Kimila Julai 6, 2026. Kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Misungwi Bi. Johari Simizi. (PICHA ZOTE NA WIZARA YA ARDHI)



Na Mwandishi Wetu
NAIBU Waziri wa Uchukuzi, David Kihenzile, ameitaka Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kuharakisha mchakato wa kufanya marekebisho ya Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma ili iendane na mabadiliko ya sasa na kugusa kada zote nyeti zinazoshiriki kufanya maamuzi muhimu serikalini.

Kihenzile alisema hayo alipotembelea banda la Sekretarieti ya Maadili katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba), yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Dar es Salaam.

Alisema pamoja na Sheria ya Maadili ya mwaka 1995 kubainisha viongozi wanaopaswa kuzingatia masharti yake, bado kuna watumishi wengi wa umma wanaoshughulikia maamuzi nyeti lakini hawapo ndani ya wigo wa sheria hiyo.

"Sekretarieti ya Maadili inapaswa kuharakisha mabadiliko ya sheria ili izifikie kada zote nyeti. Kuna watumishi ambao si viongozi kwa mujibu wa sheria, lakini wanafanya maamuzi nyeti kuliko hata mimi kama Mbunge, mfano waliopo bandarini," alisema Kihenzile.

Naye mwananchi aliyefika katika banda hilo, Samson Alphonce aliishauri Sekretarieti ya Maadili kupanua utoaji wa elimu kwa kuwafikia viongozi wote kuanzia ngazi ya kitongoji hadi viongozi wa taasisi za umma na binafsi.

Alisema elimu ya maadili ikitolewa kwa wananchi kuanzia ngazi za chini itasaidia kuongeza uelewa kuhusu majukumu ya Sekretarieti ya Maadili, kuimarisha uwazi na kuwajengea wananchi imani katika mifumo ya uwajibikaji.

"Mimi sikuwa najua kuwa kuna Baraza la Maadili linalosikiliza mashauri ya viongozi wanaokiuka maadili kama ilivyo mahakama. Mitaani wengi tunafahamu mabaraza ya ardhi pekee. Elimu ikiendelea kutolewa, wananchi wengi wataelewa zaidi kazi za taasisi hii," alisema Manyamama.

Kwa upande wake, Afisa Maadili, Grace Matunda, alisema kwa sasa Sekretarieti inaendelea kusimamia utekelezaji wa Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma ya mwaka 1995, ambayo inawahusu viongozi waliotajwa na sheria hiyo.

Aliongeza kuwa pamoja na jukumu hilo, taasisi imeongeza juhudi za kutoa elimu ya maadili kwa wananchi kupitia mikutano ya vijiji, huku pia ikifundisha somo la maadili shuleni na kuanzisha klabu za maadili kuanzia shule za msingi hadi vyuo vikuu.

Alisema hatua hizo zinalenga kujenga jamii inayozingatia maadili, uwajibikaji na uadilifu, sambamba na kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu wajibu wa viongozi wa umma na nafasi ya Sekretarieti katika kusimamia maadili nchini.


Na Mwandishi Wetu
BARAZA la Taifa la Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (NACTVET) limewahimiza wazazi na walezi kuwapeleka watoto wao katika shule zenye mkondo wa elimu ya amali, likieleza kuwa ndiyo njia sahihi ya kuandaa nguvu kazi yenye ujuzi itakayochochea maendeleo ya uchumi wa Taifa

Wito huo umetolewa na Katibu Mtendaji wa NACTVET, Dkt. Mwajuma Lingwanda, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba), yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Dar es Salaam.

Dkt. Lingwanda alisema maonesho hayo yamekuwa jukwaa muhimu kwa NACTVET kusogeza huduma karibu na wananchi kwa kutoa elimu kuhusu majukumu ya Baraza, huduma mbalimbali zinazotolewa pamoja na kupokea maoni na ushauri wa kuboresha utendaji wake.

"Maonesho haya yanatupa nafasi ya kuwafikia wananchi moja kwa moja, kuwaelimisha kuhusu elimu ya ufundi na mafunzo ya ufundi stadi pamoja na huduma zinazotolewa na Baraza. Pia tunapata fursa ya kusikiliza maoni yao ili kuendelea kuboresha huduma zetu," alisema.

Alisema NACTVET imeridhishwa na mwitikio mkubwa wa wananchi wanaotembelea banda lake, ambapo wengi wamepata taarifa na huduma walizokuwa wakizihitaji kuhusu fursa zilizopo katika sekta ya elimu ya ufundi na mafunzo ya amali.

Dkt. Lingwanda alibainisha kuwa moja ya vivutio vikubwa katika banda la NACTVET mwaka huu ni ushiriki wa wanafunzi wa shule za amali wanaoonesha kwa vitendo ujuzi walioupata kupitia kazi mbalimbali za ubunifu na uzalishaji.

Alieleza kuwa uwezo unaooneshwa na wanafunzi hao unathibitisha kuwa elimu ya amali huwajengea wahitimu uwezo wa kuingia moja kwa moja katika soko la ajira au kujiajiri mara wanapomaliza masomo yao.

"Hawa vijana wanaonesha kwa vitendo matokeo ya elimu wanayoipata. Hii ni ishara kwamba elimu ya amali inawajengea uwezo wa kufanya kazi, kuzalisha na kujitegemea mara baada ya kuhitimu," alisema.

Alisisitiza kuwa mafunzo ya ufundi na elimu ya amali yana mchango mkubwa katika kuzalisha wataalamu wenye ujuzi wa kujiajiri, kuajiriwa, kubuni teknolojia mpya na kuongeza thamani ya bidhaa zinazozalishwa nchini.

Aidha, aliwataka wawekezaji na wadau wa sekta ya elimu kutumia fursa zilizopo kuanzisha shule na taasisi zinazotoa elimu ya amali na mafunzo ya ufundi stadi, akibainisha kuwa NACTVET ipo tayari kutoa ushauri na kuwaelekeza kuhusu taratibu zote zinazohitajika.

Akizungumzia mchango wa sekta hiyo katika maendeleo ya Taifa, Dkt. Lingwanda alisema elimu ya ufundi na mafunzo ya amali ni nguzo muhimu katika kufanikisha Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kwa kujenga nguvu kazi yenye ujuzi, ubunifu na uwezo wa kuongeza uzalishaji, biashara na maendeleo ya viwanda.

Aliongeza kuwa wingi wa bidhaa zinazozalishwa na Watanzania na kuoneshwa katika Maonesho ya Sabasaba ni ishara kuwa nchi inaendelea kujenga uchumi unaotegemea uzalishaji na ujuzi wa wananchi wake, hali inayochochea ajira, ukuaji.


Na Mwandishi Wetu
RAIS  na Mkurugenzi Mkuu wa Octant Energy, Richard Schmitt, amesema Kampuni hiyo bado ina dhamira ya dhati kuendelea kuwekeza nchini kwa kuzingatia sheria viwango vya kitaalamu na maslahi ya wananchi.

Akizungumza katika banda la Mamlaka ya Udhibiti Mkondo wa Juu wa Petroli (PURA) kwenye Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara Sabasaba, Schmitt amesema kampuni hiyo inaendelea kutekeleza shughuli zake kwa kushirikiana kwa karibu na PURA pamoja na wadau wengine.

Akiwa katika banda la PURA, Schmitt amepata elimu kuhusu mfumo wa usimamizi wa shughuli za utafutaji, uendelezaji na uzalishaji wa mafuta na gesi asilia nchini pamoja na kuhakikisha rasilimali za Petroli zinazoendelezwa zinazingatia sheria, na uwazi.

Octant Energy ni waendeshaji wa Kitalu cha Uchimbaji Tanga ambao wamefika katika banda la PURA kwenye maonesho ya Sabasaba kama moja ya wadau wa PURA. 



 


*Aipongeza TASAC kutoa gawio la Zaidi ya sh.bilioni 20

Na Mwandishi Wetu
SERIKALI imeihakikishia sekta ya usafiri wa majini kuwa itaendelea kulinda uwekezaji wa vyombo vya majini na mali za wawekezaji ili kuimarisha mazingira salama ya biashara, huku ikiitaka Tanzania Shipping Agencies Corporation (TASAC) kuongeza juhudi katika kuzalisha wataalamu wa sekta ya bahari ili kukidhi mahitaji yanayoongezeka.

Kauli hiyo imetolewa na Naibu Waziri wa Uchukuzi, David Kihenzile, baada ya kutembelea banda la TASAC katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere.

Kihenzile amesema Serikali imejipanga kuhakikisha wawekezaji wanaowekeza katika meli, boti na vyombo vingine vya majini wanaendelea kufanya shughuli zao kwa usalama, huku ulinzi wa wananchi, wageni na mali zao ukipewa kipaumbele kupitia taasisi husika.

Amesema mazingira hayo salama yataendelea kuongeza imani ya wawekezaji na kuvutia uwekezaji zaidi katika uchumi wa buluu, ambao ni moja ya sekta muhimu zinazochochea ukuaji wa uchumi wa Taifa na kuongeza fursa za ajira kwa Watanzania.

Katika hatua nyingine, Kihenzile ameipongeza TASAC kwa mafanikio yake ya kifedha baada ya kutoa gawio la Shilingi bilioni 20.45, sawa na asilimia 15 ya mapato ghafi ya shirika kwa mwaka wa fedha 2025/26, ambalo lilikabidhiwa kwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Amesema kiwango hicho cha gawio kinaonyesha shirika linafanya kazi kwa ufanisi na kuwataka viongozi na watumishi wake kuendelea kusimamia majukumu yao kwa weledi na uwajibikaji ili kuongeza mchango wa taasisi hiyo katika uchumi wa Taifa.

Akizungumzia ukuaji wa sekta ya usafiri wa majini, Kihenzile amesema ongezeko kubwa la biashara katika bandari za Tanzania limeongeza mahitaji ya wataalamu wa sekta ya bahari, akibainisha kuwa kiwango cha mizigo kilichokuwa kinatarajiwa kufikiwa mwaka 2030 kilifikiwa mapema mwaka 2022 kutokana na uongozi madhubuti, kuimarika kwa diplomasia ya uchumi na ushiriki wa sekta binafsi.

Amesema ukuaji huo unamaanisha kuwa kutahitajika idadi kubwa zaidi ya manahodha, mabaharia, wasaidizi wa mabaharia pamoja na wataalamu wengine wa usafiri wa majini ili kuhudumia shughuli zinazozidi kupanuka.

Kutokana na hali hiyo, ameihimiza TASAC kutotekeleza jukumu la udhibiti pekee, bali kushirikiana na Serikali kuweka mikakati madhubuti ya kuzalisha wataalamu wa kutosha watakaoweza kukidhi mahitaji ya sekta ya bahari inayokua kwa kasi.

Aidha, amewapongeza watumishi wa TASAC kwa uadilifu na weledi wanaouonyesha katika utekelezaji wa majukumu yao, akiwataka kuendelea kufanya kazi kwa uzalendo ili kuhakikisha sekta ya bahari inatoa manufaa makubwa kwa Watanzania na kuchangia maendeleo endelevu ya Taifa.






Top News