NA Janeth Raphael MichuziTv Bungeni Dodoma.
Mbunge wa Katavi, Thomas Maganga ameipongeza Wizara ya Viwanda na Biashara kwa kile alichodai kuwa ni kazi kubwa na nzuri inayofanywa katika kukuza sekta ya biashara na uwekezaji nchini, huku akimtaka Waziri wa wizara hiyo, Judith Kapinga kuweka nguvu zaidi katika kulinda wafanyabiashara wa ndani dhidi ya ushindani kutoka kwa wafanyabiashara wa kigeni.
Akichangia hoja ya makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Viwanda na Biashara kwa mwaka wa fedha 2026/2027 leo Bungeni jijini Dodoma, Maganga alisema historia itamkumbuka Waziri Kapinga iwapo atasimamia kwa uthabiti maslahi ya wafanyabiashara wazawa na kuhakikisha wanapata mazingira rafiki ya kufanya biashara na kuwekeza nchini.
“Dada yangu hakuna kitu ambacho taifa litakukumbuka kama kulinda wafanyabiashara wa ndani,” alisema Maganga huku akisisitiza kuwa ukuaji wa uchumi wa taifa unapaswa kuwanufaisha zaidi Watanzania wenyewe.
Mbunge huyo amesema ipo haja ya Serikali kuweka mifumo madhubuti ya kudhibiti ongezeko kubwa la wafanyabiashara wa kigeni wanaoingia nchini na kufanya shughuli ambazo zinaweza kufanywa na wazawa, akieleza kuwa hali hiyo imekuwa changamoto kwa wafanyabiashara wengi wa ndani kushindana kwenye soko.
Amesema pamoja na umuhimu wa uwekezaji kutoka nje ya nchi, Serikali inapaswa kuweka mkazo mkubwa katika kuwajengea uwezo wawekezaji wa ndani ili waweze kuwa nguzo ya uchumi wa taifa kwa muda mrefu.
Katika mchango wake huo, Maganga pia aliwataka wafanyabiashara na wawekezaji wa Kitanzania kutumia fursa zilizopo kuwekeza zaidi ndani ya nchi, akisema hatua hiyo inaweza kusaidia kupunguza tatizo la ajira kwa kiwango kikubwa katika miaka michache ijayo.
“Wawekezaji wa ndani wakiamua kuwekeza kwa nguvu nchini, naamini ndani ya miaka mitano ijayo changamoto ya ukosefu wa ajira itapungua kwa kiasi kikubwa,” alisema.
Aidha, Maganga ameeleza kuwa baadhi ya wawekezaji wa kigeni wamekuwa wakinufaika zaidi na rasilimali na fursa za ndani bila kuacha manufaa makubwa kwa taifa, hali inayozua mjadala kuhusu namna bora ya kusawazisha uwekezaji wa ndani na wa nje.
“Hao wawekezaji wa nje wanakuja na fedha kidogo lakini wakishafanikiwa wanaondoka na faida kubwa, wakati mwingine wakituachia changamoto mbalimbali katika jamii,” alisema.
Kauli ya mbunge huyo imeibua mjadala kuhusu umuhimu wa Serikali kuendelea kuweka sera na mikakati itakayowezesha wafanyabiashara wa ndani kukua, kuhimili ushindani wa soko na kuchangia kikamilifu katika maendeleo ya uchumi wa nchi.
Wizara ya Viwanda na Biashara imekuwa ikiwasilisha bungeni mikakati mbalimbali inayolenga kukuza viwanda vya ndani, kuongeza uzalishaji wa bidhaa za Kitanzania pamoja na kuvutia uwekezaji wenye tija kwa taifa.




.jpeg)


.jpg)

.jpeg)



.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)








.jpeg)

.jpeg)


