Mkurugenzi Mtendaji wa Jukwaa la Watendaji Wakuu nchini (CEO Roundtable of Tanzania-CEOrt) B. Santina Benson (kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Wanawake Wafanyabiashara Tanzania (TWCC) Dkt. Mwajuma Hamza  wasaini Hati ya Makubaliano (MoU) kwa ajili ya kushirikiana katika kuwawezesha wafanyabishara wanawake kukua kiuchumi kupitia mpango wa CEOrt unaojulikana kama ‘Think Equal, Lead Smart (TELS), ulioanzishwa mwaka 2024 kwa kushirikiana na Vodacom Tanzania Foundation.Hafla hiyo imefanyika katika hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam Ijumaa Februari 6, 2026
Mkurugenzi Mtendaji wa Jukwaa la Watendaji Wakuu nchini (CEO Roundtable of Tanzania-CEOrt) B. Santina Benson (kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Wanawake Wafanyabiashara Tanzania (TWCC) Dkt. Mwajuma Hamza, mara baada ya kusaini Hati za Makubaliano (MoU) kwa ajili ya kushirikiana katika kuwawezesha wafanyabishara wanawake kukua kiuchumi kupitia mpango wa CEOrt unaojulikana kama ‘Think Equal, Lead Smart (TELS), ulioanzishwa mwaka 2024 kwa kushirikiana na Vodacom Tanzania Foundation. Hafla hiyo imefanyika katika hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam Ijumaa Februari 6, 2026.

Meneja wa Vodacom Tanzania Foundation, Bi. Sandra Oswald, akisisitiza  jambo wakati wa mwendelezo wa mkutano wa program ya Jukwaa la Watendaji Wakuu nchini ( CEO Roundtable of Tanzania- CEOrt)  inayojulikana kama ‘Think Equal, Lead Smart (TELS), ilioanzishwa mwaka 2024 kwa kushirikiana na Vodacom Tanzania Foundation, kwa lengo la kukuza usawa wa fursa kwa wanawake katika uongozi, biashara na nafasi za maamuzi.

Na Mwandishi Wetu
JUKWAA  la Wakurugenzi Wakuu Tanzania (CEO Roundtable of Tanzania-CEOrt) na Chama cha Wanawake Wafanyabiashara Tanzania (TWCC) kwa pamoja wamesaini Hati ya Makubaliano (MoU) ili kurasimisha ushirikiano wa kimkakati unaolenga kuharakisha uongozi na ushiriki wa wanawake katika shughuli za kiuchumi hapa nchini.

Ushirikiano huo utatekelezwa kupitia mpango wa CEOrt unaojulikana kama ‘Think Equal, Lead Smart (TELS), ulioanzishwa mwaka 2024 kwa kushirikiana na Vodacom Tanzania Foundation, kwa lengo la kukuza usawa wa fursa kwa wanawake katika uongozi, biashara na nafasi za maamuzi.

Kupitia ushirikiano huu, CEOrt na TWCC zitafanya kazi kwa pamoja kuimarisha biashara za wanawake ,ikiwemo biashara ndogo, ndogo sana na za kati (MSMEs)—kwa kuwajengea wanawake ujuzi wa uongozi, biashara na matumizi ya teknolojia za kidijitali, kuongeza utayari wa kukua kifedha, na kushughulikia vikwazo katika kijamii vinavyokwamisha maendeleo yao kiuchumi.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo ya utiaji saini iliyofanyika katika Hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mtendaji wa CEOrt, Bi. Santina Benson, alisisitiza umuhimu wa kushughulikia changamoto za kimfumo zinazoendelea kuzuia ushiriki kamili wa wanawake katika masuala ya kiuchumi na uongozi.

“Think Equal, Lead Smart imebuniwa kuunganisha wajasiriamali wanawake na mifumo ya sera, uwekezaji na uongozi na ushirikiano huu kati ya CEOrt na TWCC unaimarisha uwezo wetu wa kuwasaidia wanawake wanaojihusisha na shughuli za kiuchumi katika mikoa mbalimbali na kuhakikisha wanawake wanajumuishwa kikamilifu katika mifumo ya maendeleo na uongozi wa Tanzania,” alisema .Santina

Hata hivyo alibainisha kuwa MoU hiyo itafungua njia za upatikanaji wa mitaji, masoko na ushauri wa kibiashara kupitia wanachama wa CEOrt na washirika wa kimkakati. Miunganisho hiyo inatarajiwa kuongeza fursa kwa wanawake kupata mitaji, kuingia katika minyororo ya thamani ya juu zaidi, na kunufaika na mwongozo wa kibiashara pamoja na mitandao ya sekta mbalimbali.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa TWCC, Dkt. Mwajuma Hamza, alisema kuwa ushirikiano huo unashughulikia changamoto halisi zinazowakabili wanawake wajasiriamali nchini.

“Wanachama wetu bado wanakabiliwa na changamoto za upatikanaji wa mitaji, masoko, ushauri wa kitaalamu na nafasi za maamuzi. Ushirikiano huu na CEOrt unatoa fursa za vitendo kwa wanawake kujenga biashara endelevu, kupata nafasi za uongozi na kushindana kikamilifu katika uchumi,” alisema.

Ushirikiano huo ulitanguliwa na kikao cha kwanza cha maarifa cha Think Equal, Lead Smart, kilichowakutanisha viongozi wa biashara, washirika wa maendeleo, watunga sera na wanawake wajasiriamali jijini Dar es Salaam.

Kikao hicho kilifanyika katika Hoteli ya Serena chini ya kaulimbiu “Mustakabali wa MSMEs Zinazoongozwa na Wanawake: Ushirikishwaji, Changamoto na Fursa. Lengo ni kuwawezesha wanawake wajasiriamali kushiriki kikamilifu katika ajenda ya maendeleo ya muda mrefu chini ya Dira ya Maendeleo ya Tanzania 2050 (DIRA 2050).

Jukwaa la TELS lilibuniwa kukuza ushiriki jumuishi wa kiuchumi kwa kuhimiza majadiliano kati ya sekta binafsi, taasisi za kifedha, watunga sera na MSMEs zinazoongozwa na wanawake. Kupitia ubadilishanaji wa maarifa na majadiliano yanayoongozwa na sera, mpango huu unalenga kuwaweka wanawake wajasiriamali kama wahimili muhimu wa mabadiliko ya kiuchumi nchini.

Akizungumza katika jukwaa hilo, Meneja wa Vodacom Tanzania Foundation, Sandra Oswald, alisisitiza umuhimu wa kujenga mifumo itakayowezesha biashara zinazoongozwa na wanawake kukua, kurasimishwa na kushindana kwa uendelevu.

“MSMEs zinazoongozwa na wanawake ndizo mhimili wa uchumi wa Tanzania, zikichangia kwa kiasi kikubwa ajira, kipato cha kaya na ubunifu wa ndani. Hata hivyo, bado zinakabiliwa na vikwazo vya kimfumo vinavyozuia ukuaji wao. Ili Tanzania ifikie malengo ya Dira ya 2050, wanawake wajasiriamali lazima wajumuishwe kikamilifu katika mkakati wa ukuaji wa uchumi wa taifa,” alisema.

Kikao hicho kilitoa fursa kwa wanawake wajasiriamali kueleza wazi changamoto wanazokumbana nazo, ikiwemo ukosefu wa mitaji nafuu, changamoto za matumizi ya teknolojia za kidijitali, vikwazo vya kisheria na kiutawala, upungufu wa masoko na mifumo dhaifu ya msaada wa biashara.

Sandra alieleza kuwa kuoanisha majadiliano ya TELS na Dira ya 2050 kunazitambua MSMEs zinazoongozwa na wanawake kama nguzo muhimu za mabadiliko ya kiuchumi, ubunifu na ukuaji jumuishi.

Ikiwa katika hatua kwanza katika mipango mbalimbali iliyopangwa katika utekelezaji wake, jukwaa la maarifa la Think Equal, Lead Smart litaendelea kuwakutanisha wadau kwa ajili ya kubadilishana mawazo yanayotekelezeka, suluhisho za vitendo na mikakati inayooana na sera za kitaifa. Vikao vijavyo vinatarajiwa kufanyika katika mikoa na sekta mbalimbali, vikisisitiza nafasi ya MSMEs zinazoongozwa na wanawake kama wachangiaji wakuu wa ustawi wa taifa.

Shirika la Wanawake katika Sheria na Maendeleo Barani Afrika (WiLDAF Tanzania), kwa kushirikiana na mtandao wa kupambana na ukatili wa kijinsia (Mkuki) na wadau wengine wa maendeleo, wameandaa na kugawa tuzo kwa vinara 16 wa kupinga vitendo vya ukatili wa kijinsia na utetezi wa haki za binadamu.


Ugawaji wa tuzo hizo umefanyika Februari 05, 2026 jijini Dar es salaam na kuhudhuriwa na wawakilishi wa serikali, mabalozi mbalimbali, mashirika ya Umoja wa Mataifa, wanaharakati wa haki za wanawake, wanasheria, vyombo vya habari na asasi za kiraia,


Akizungumza katika Hafla hiyo, Mkurugenzi wa WiLDAF Tanzania, Wakili Anna Kulaya, alisisitiza kuwa juhudi za kupambana na ukatili wa kijinsia kwa wanawake na watoto ni jukumu letu sote ikiwa ni Pamoja na kuwasaidia wote waliopitia ukatili huo. Huku akipongeza hatua ya jamii kubwa ambayo kwasasa haikalii kimya ukatili wa kijinsia kwa wanawake na watoto.

“Tumeona viongozi wa jamii wanabadili fikra na kuwa sehemu ya jitihada zetu za kuukata ukatili wa kijinsia hasa baadhi ya mila potofu. Tumeona kuongezeka kwa uelewa wa haki za kisheria na haki za binadamu kiujumla. Kwasasa wanajamii wengi wanavunja ukimya dhidi ya vitendo hivi, wanachukua hatua kudai haki na uwajibikaji”,amesema


Aidha, amepongeza juhudi za serikali katika kuunga mkono mapambano hayo ya uimarishwaji wa mifumo ya utoaji haki ikiwa ni Pamoja na kuongeza idadi ya madawati ya kijinsia, Pamoja na kuongezeka kwa weledi wa kuwahudumia waathirika na wahanga wa vitendo vya ukatili huo.


“Tumeona uimarishwaji wa mifumo ya utoaji haki ikiwa ni Pamoja na kuongeza idadi ya madawati ya kijinsia, Pamoja na kuongezeka kwa weledi wa kuwahudumia waathirika na wahanga wa vitendo vya ukatili huo”, ameongeza Kulaya.


Bi. Kulaya ametumia nafasi hiyo kuwashukuru wadau wa maendeleo waliounga mkono kufanikisha zoezi la ugawaji tuzo hizo ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha haki za wanawake na watoto, wadau hao ni Ubalozi wa Uswisi, Ubalozi wa Finland, ubalozi wa Ireland, UNFPA, UNICEF, LSF,BRAC, ITV, Coca-Cola Kwanza Ltd, na TBL.









































Na Seif Mangwangi, Michuzi TV Arusha

ONGEZEKO la vitendo vya ukatili na uhalifu vinavyoendelea nchini ni matokeo ya ukosefu wa mfumo wa malezi na makuzi bora ya watoto tangu wakiwa wadogo, wakati Mama akiwa mjamzito na baada ya kuzaliwa.

Hayo yameelezwa leo 6 Februari 2026 na Afisa ustawi wa jamii Mkoa wa Arusha, Denis Mgiye alipokuwa akizungumza na Waandishi wa habari wakati wa mafunzo kuhusu mpango wa makuzi na malezi kwa baadhi ya waandishi wa habari Mkoa wa Arusha yanayoendelea katika mji wa Karatu.

Migiye ambaye pia ni mratibu wa mpango wa malezi na makuzi ya mtoto Mkoa wa Arusha, amesema mtoto tangu akiwa mimba na baada ya kuzaliwa anapaswa kupewa malezi bora ya Baba na Mama Ili kumkuza katika hali bora na kumjenga kiakili, kimaadili, afya, elimu na usalama.

“ Watoto wengi wanaharibika wakiwa bado wadogo baada ya kukosa malezi bora akiwa katika hatua za makuzi, mtoto anatakiwa kusemeshwa tangu akiwa mimba na hata baada ya kuzaliwa,” amesema.

Amesema takwimu zinaonyesha kuwa watoto wenye umri wa miaka 4 na 5 ukuaji wao umekuwa kwa asilimia 65 jambo ambalo linarudisha nyuma mfumo mzima wa maisha ya mtoto.

Afisa kutoka taasisi ya SOS ambao ndio wafadhili wakuu wa mafunzo hayo,Husna Selungwi  amesema wamekutanisha waandishi kupitia program ya Arusha Innovation Ili kusaidia kusambaza elimu ya makuzi na malezi kwa jamii.

Amesema katika Mkoa wa Arusha na maeneo mengine nchini watu wengi wamekuwa hawana elimu ya makuzi na ndio sababu mtoto akikua matatizo mengi yanakuwa yanaibuka ikiwemo kufeli kielimu.

“ umri wa awali wa watoto kwenda elimu ya awali imekuwa ni ndogo tofauti na miongozo ya kitaifa inavyoelekeza, hili linajitokeza Kwa sababu wazazi hawana elimu ya makuzi na malezi, tumeita waandishi wa habari kuwapa elimu hii Ili tusaidiane kutoa elimu zaidi Kwa jamii kupitia kalamu zenu,” amesema na kuongeza:

“ Tunahitaji nguvu kubwa zaidi kutoa elimu ndio sababu tunatumia vyombo vya habari kuendeleza kusisitiza umuhimu wa malezi Bora Kwa watoto,” amesema.

Awali akifungua mafunzo hayo, Mwenyekiti wa Chama cha Waandishi wa Habari Mkoa wa Arusha, Claud Gwandu amewataka waandishi wanaoshiriki mafunzo hayo kuyazingatia Ili kujenga jamii Bora na sikivu.

Amesema mafunzo hayo ni muhimu kwa waandishi wa habari kwa kuwa na wao  pia ni walezi, na hivyo kuwataka kutumia mafunzo hayo kama fursa.

“ Tumepata nafasi hii tuitumie kama fursa, na kuacha kufanya mambo kwa mazoea, kwa Sasa taaluma yetu umebanwa sana, tukipata fursa kama hizi ndio tunapaswa kuzitumia kujijenga na kuigeuza kuwa sehemu ya kupata kipato, ukiwa unaandika habari za watoto na wewe utaonekana huko duniani hiyo ni fursa,” amesema.







Top News