NI miaka 30 tangu kuanzishwa kwa Taasisi ya Saratani nchini Tanzania (Ocean Road). Kuanzishwa kwake kumeleta matumaini ya kuendelea kuishi kwa mamilioni ya wananchi.

Kila safari kubwa huanza na maono, matumaini, ujasiri na imani kwamba hata katika nyakati ngumu maisha yanaweza kulindwa. Mwaka 1996, katika changamoto za kiafya na rasilimali chache, wazo moja lilizaliwa si kwa hofu bali kwa maarifa, huruma na uthubutu.

Haikuwa rahisi kuanza safari hiyo ngumu, lakini taasisi hiyo ilijengwa kwa dhamira thabiti ya kuhudumia watu.

Dkt. Hamza Maunda anasimulia kuwa hali ilikuwa ngumu kwa kuwa taasisi ilianza ikiwa na uhaba wa wafanyakazi na vifaa tiba kwa ajili ya matibabu ya saratani.

“Taasisi hiyo iliendelea kuimarika siku hadi siku mpaka kufikia hatua ya kuwa na wataalamu waliosoma ndani ya taasisi hiyo,” alisema.

“Pamoja na changamoto zote, tuliweza kujijenga siku hadi siku, na mwaka 2013 taasisi ilianzisha masomo ya kuwafundisha madaktari kubobea katika eneo la saratani; hiyo ilikuwa hatua muhimu sana,” aliongeza Dkt. Maunda

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Saratani Ocean Road, Dkt. Diwani Msemo, akieleza mafanikio ya taasisi hiyo amesema yametokana na uwekezaji wa serikali.

“Rais Samia, kwa kipindi cha miaka yake minne ya awamu ya sita, aliwekeza zaidi ya shilingi milioni 40 kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya matibabu ya saratani,” alisema Dkt. Msemo.

Amesema kuwa jitihada za serikali ziliipa nguvu taasisi hiyo, hususan Wizara ya Afya, kuanzisha mpango maalumu wa kushughulikia saratani.

Ameeleza kuwa mafanikio ya Ocean Road yameifanya serikali kuongoza jitihada za makusudi za kuwasogezea wananchi huduma hizo.

“Wananchi walikuwa wakisafiri umbali mrefu, wengine kilometa 1,000 hadi 1,300, kufuata huduma hii. Serikali ikaona iwasogezee wananchi huduma hiyo karibu,” alisema.

Dkt. Yokebeth Vuhahula, daktari bingwa wa saratani, amesema awali taasisi hiyo ilikuwa inategemea wagonjwa kupimwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili kabla ya kupelekwa kutibiwa Ocean Road.

“Tulikuwa hatuna idara ya Patholojia, ambayo ni muhimu sana katika taasisi za saratani kwa maana ndicho kipimo kinachoonesha kama mgonjwa ana saratani. Tulikuwa tunasubiri wagonjwa wapimwe Muhimbili, lakini sasa vipimo vinafanyika hapa,” alisema.

Mwanga Mhoka, mtaalamu wa vipimo vya Patholojia, amesema taasisi hiyo imepiga hatua zinazoonekana kwa macho.

“Tumepiga hatua kubwa; tulikuwa na wauguzi wachache na vifaa vichache, lakini sasa mambo ni mazuri,” alisema.

Dkt. Jasmin Salum ni mmoja wa waliopona saratani baada ya kufika katika taasisi hiyo.

“Nilipoambiwa nina saratani nilijua tayari maisha yameisha, lakini taasisi hii imenirudishia tumaini la kuendelea kuishi,” alisema.

Naye Babu wa Kitaa, mtangazaji wa Clouds Media Group, ni shuhuda wa matibabu ya taasisi hiyo, akiwa ni mmoja wa wagonjwa waliohudumiwa na kupona.

“Kwanza namna nilivyohudumiwa hapa, kuanzia kwa wauguzi mpaka kwa madaktari, ilikuwa huduma nzuri sana, yenye ukarimu na uweledi wa hali ya juu,” alisema.

Babu wa Kitaa amesema kilichompa matumaini zaidi ni kuona watu wengi waliokoa maisha yao katika taasisi hiyo.

“Hapo ndipo nilielewa kuwa Ocean Road ina nafasi kubwa ya kubadilisha maisha ya watu wengi ambao hawana uwezo wa kwenda nje ya nchi kupata matibabu,” alisema.

Ameongeza kuwa kwa sasa nchi jirani zinakimbilia Ocean Road si kwa sababu ya jina, bali kwa sababu ya ubora wa huduma.
WAKATI Chama Cha Mapinduzi(CCM) leo Februari 5,2026 kikitimiza miaka 49 tangu kuanzishwa kwake Februari 5,1977 wanachama, mashabiki, wapenzi na wadau mbalimbali wameungana na Chama hicho katika kusherekea.

Hata hivyo pamoja na kuadhimisha kwa sherehe hizo Kada wa Chama Cha Mapinduzi na mdau wa maendeleo nchini, Nathan Kimaro ameungana na Wana CCM kusherekea miaka 49 ya Chama hicho ambapo pia ametoa ushauri wenye lengo la kujenga Chama imara zaidi.

Katika ushauri wake anesema kila taasisi kubwa hufika wakati wa kujitathmini. Hivyo siku hii iwe si ya kusherehekea miaka pekee, bali ya kuhuisha dhamira.

Amesema "Wakati umefika tuwe ni Chama ambacho unyenyekevu uwe dira yetu chama cha kutoa matumaini, kurejesha furaha, na kuacha alama ya Utu,Huduma na kusimamia haki na stahiki za wananchi.

"Tuiunganishe nchi yetu, tuwe sehemu ya mchakato wa uponyaji, na tuwape watu sababu ya kutabasamu tena.

"Ni wakati wa kurudisha kwa wale waliotuamini kwa miaka yote, 𝗸𝘄𝗮 𝗞𝘂𝗮𝗻𝘇𝗶𝘀𝗵𝗮 𝗖𝗖𝗠 𝗙𝗢𝗨𝗡𝗗𝗔𝗧𝗜𝗢𝗡."

Amesema Foundation hiyo ya Chama ni kwa ajili ya kuwahudumia wasio na sauti, kukuza vijana, wanawake, haki za watoto, elimu pamoja na kusaidia wagonjwa,yatima, wajane, na wanaoonewa.

Pia kutoa misaada ya kimaisha, na kuleta uso mpya wa CCM kwamba sio tu jukwaa la siasa pia Chama cha huduma kwa watu wa kada zote.

"Nyimbo mpya si nyimbo za majivuno au mashindano na kiburi, kama “CCM ni ile ile” au “wachawaseme CCM ina wenyewe” bali nyimbo za uzalendo, motisha, na maendeleo,nyimbo zitakazolisukuma kilimo na kauli mbiu za Umoja.

"Tuvae katika uvaaji wa ukaribisho na urafiki, tuwatazame upande wa pili kwa jicho la tabasamu na hata wanapokosea kwa mipango miovu na ukosofu wa Nidhamu, CCM Kama chama Baba na Mama kiwatazame kwa jicho la Mlezi kwa Mtoto mkosaji,

"Tujenge chama chenye umoja na nidhamu ya ndani. Kwa njia hii, CCM haitabaki kuwa historia bali itaendelea kuwa ahadi hai ya taifa. Na kuyaishi maneno ya Baba wa Taifa ya CCM madhubuti.

Heri ya Siku ya Kuzaliwa chama changu CCM."








Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) Wilaya ya Ilala, chini ya Mwenyekiti wake Ndg. Neema Kiusa, imeadhimisha miaka 49 ya kuzaliwa kwa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwa kutembelea Kituo cha Kulea Watoto Yatima cha Upendo Orphanage Centre, kilichopo Buguruni Kisiwani (Ghana), jijini Dar es Salaam.

Katika maadhimisho hayo, UWT Wilaya ya Ilala ilitoa msaada wa vitu mbalimbali kwa watoto wanaolelewa katika kituo hicho, ikiwa ni sehemu ya kuonesha mshikamano, upendo na uwajibikaji wa kijamii kwa makundi yenye mahitaji maalumu.

Aidha, watoto wa Kituo cha Upendo Orphanage Centre kwa kushirikiana na wanachama wa UWT Wilaya ya Ilala walifanya dua maalum kuliombea Taifa letu, pamoja na kumuombea Mwenyekiti wa CCM Taifa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, ili aendelee kuliongoza Taifa kwa hekima na busara.

Kwa pamoja waliomba amani, umoja na mshikamano wa Taifa, wakisisitiza umuhimu wa kuilinda na kudumisha amani ya nchi yetu.






Wakala wa Maendeleo ya Usimamizi wa Elimu (ADEM) kwa kushirikiana na VVOB – Education for Development umefikia hatua muhimu katika kuimarisha uongozi wa shule nchini Tanzania kufuatia utekelezaji wenye mafanikio wa Mradi wa LIT-LEAD.

Kupitia mradi huo, timu ya wataalamu wa elimu ilifanya zoezi la kina la ukusanyaji wa takwimu katika mikoa sita ya Tanzania Bara ambayo ni Mbeya, Singida, Katavi, Simiyu, Manyara na Morogoro, kwa lengo la kutathmini hali ya sasa ya uongozi wa shule na kubaini maeneo ya kipaumbele yanayohitaji kuboreshwa.

Mradi huo pia umefanikisha uandaaji wa miongozo ya mafunzo ya vitendo na inayozingatia mazingira halisi ya shule, ambayo sasa iko tayari kutumika katika kuwajengea uwezo wakuu wa shule za sekondari nchini Tanzania Bara. Miongozo hiyo imelenga kuimarisha ujuzi wa uongozi, usimamizi na usimamizi wa ufundishaji (instructional supervision), hatua itakayochangia kuboresha ufundishaji na ujifunzaji shuleni.

Akizungumza katika kikao cha mapitio ya mradi, Mtendaji Mkuu wa ADEM, Dkt. Maulid J. Maulid, aliusifu ushirikiano imara kati ya ADEM na VVOB, akieleza kuwa ni wa wakati muafaka na wenye matokeo chanya.

“Ushirikiano huu kati ya ADEM na VVOB ni wa kimkakati. Umeweka msingi thabiti utakaoleta mabadiliko chanya na endelevu katika uongozi wa shule, hususan shule za sekondari nchini Tanzania,” alisema Dkt. Maulid.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Programu wa Kimataifa wa VVOB, Bw. Tom Vandenbosch, alieleza kuridhishwa na hatua iliyofikiwa katika utekelezaji wa mradi huo.

“Tumeridhishwa sana na namna ushirikiano wetu na ADEM unavyoendelea. Kazi ya awali imefanyika kwa umakini mkubwa, na tuna imani kuwa sasa tuko tayari kuanza mafunzo ya wakuu wa shule nchini Tanzania,” alisema.



Mradi wa LIT-LEAD unatarajiwa kuwa na mchango mkubwa katika kuimarisha uwezo wa uongozi miongoni mwa wakuu wa shule, jambo litakaloboresha usimamizi wa shule na kujenga mazingira bora ya ujifunzaji kwa wanafunzi kote nchini.
Na Karama Kenyunko Michuzi Tv

MAMLAKA ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imesema mikoa ya pwani ya kaskazini, baadhi ya maeneo ya magharibi mwa Ukanda wa Ziwa Victoria pamoja kaskazini inatarajiwa kupata mvua za wastani hadi juu ya wastani katika msimu wa mvua za masika(Machi -Mei), 2026.

Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi Dkt. Ladislaus Chang’a, amesema hayo leo, Februari 5, 2026 wakati akitangaza utabiri kwa waandishi wa habari kuhusu mwelekeo wa mvua na athari zinazoweza kujitokeza katika sekta mbalimbali za kijamii na kiuchumi.

"Mvua za masika zinatarajiwa kuanza wiki ya nne ya Februari na wiki ya kwanza ya Machi 2026 katika Ukanda wa Ziwa Victoria, wiki ya kwanza na ya pili ya Machi katika maeneo ya pwani ya kaskazini, na wiki ya pili hadi ya tatu ya Machi katika nyanda za juu kaskazini mashariki,"amesema Chang'a

Ameongeza,"Mvua hizo zinatarajiwa kuisha kati ya wiki ya nne ya Mei na wiki ya kwanza ya Juni mwaka huu,huku ongezeko la mvua likitarajiwa zaidi mwezi Aprili,

Amesema,TMA imetabiri kuwa mvua za wastani hadi juu ya wastani zinatarajiwa katika mikoa ya Kagera na Geita, kaskazini mwa mkoa wa Kigoma pamoja na maeneo mengi ya pwani ya kaskazini ikiwemo Dar es Salaam, Tanga, Pwani, kaskazini mwa Morogoro na visiwa vya Unguja na Pemba.

Aidha,amesisitiza kuwa mvua za wastani hadi chini ya wastani zinatarajiwa katika nyanda za juu kaskazini mashariki (Arusha, Manyara na Kilimanjaro) na baadhi ya maeneo ya Ukanda wa Ziwa Victoria ikiwemo Mwanza, Shinyanga, Mara na Simiyu.

Akieleza athari zinazoweza kujitokeza endapo, Chang’a amesema vipindi vya mvua kubwa vinaweza kusababisha mafuriko, kutuama kwa maji na uharibifu wa miundombinu katika baadhi ya maeneo, huku maeneo yatakayopata mvua chache yakikabiliwa na upungufu wa unyevu wa udongo na kushuka kwa kina cha maji katika mito na mabwawa.

“Msimu wa mvua za Masika ni mahsusi kwa maeneo ya nyanda za juu kaskazini mashariki (mikoa ya Arusha, Manyara na Kilimanjaro), pwani ya kaskazini (kaskazini mwa mkoa wa Morogoro, mkoa wa Pwani ikijumuisha visiwa vya Mafia, Dar es Salaam, Tanga pamoja na visiwa vya Unguja na Pemba), ukanda wa Ziwa Viktoria (mikoa ya Kagera, Geita, Mwanza, Shinyanga, Simiyu na Mara), pamoja na kaskazini mwa mkoa wa Kigoma,” amesema Dkt. Chang’a.

Aidha Mamlaka imewaasa wadau wa sekta mbalimbali ikiwemo kilimo, mifugo, uvuvi, afya, nishati, maji, ujenzi na usafirishaji kuzingatia utabiri huo pamoja na taarifa za hali ya hewa za kila siku na tahadhari rasmi zinazotolewa na TMA ili kupunguza athari zinazoweza kujitokeza.

Chang’a amekumbusha kuwa kwa mujibu wa Sheria ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania Na. 2 ya mwaka 2019, ni kosa kisheria kusambaza utabiri wa hali ya hewa kutoka vyanzo visivyo rasmi, na kuvitaka vyombo vya habari kuzingatia taarifa rasmi za TMA katika kuhabarisha umma.
Shirika la Viwango Tanzania (TBS) Kanda ya Kaskazini, Arusha limeteketeza tani tatu za bidhaa zisizo salama katika dampo la jiji la Arusha mapema leo.

Bidhaa zilizoteketezwa ni pamoja na vyakula ambavyo havijasajiliwa, vipodozi vyenye viambata hatarishi kwa afya, bidhaa zilizokwisha muda wake wa matumizi (expired) pamoja na nguo za ndani za mitumba.

Hatua hiyo ni sehemu ya mikakati endelevu ya TBS ya kulinda afya na usalama wa wananchi kwa kuondoa sokoni bidhaa zisizokidhi viwango vilivyowekwa.

Aidha, hatua hiyo inalenga kujenga imani ya walaji juu ya ubora wa bidhaa zinazopatikana sokoni na kuhakikisha soko la Tanzania linakuwa salama, lenye ushindani na mchango chanya katika maendeleo ya taifa.
Serikali imeiagiza Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) kubuni na kuimarisha njia rahisi za kufikisha matokeo ya tafiti kwa Wizara husika na taasisi nyingine zinazohusika, ili matokeo hayo yafanyiwe kazi na kusaidia kutatua changamoto zinazotokana na mabadiliko ya tabianchi.

Hayo yalibainishwa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Daniel Mushi, wakati wa ufunguzi wa mkutano wa kwanza wa kila mwaka wa maendeleo ya utafiti chini ya Programu ya Utafiti wa Mabadiliko ya Tabianchi.

Profesa Mushi alisema matokeo ya tafiti ni muhimu kwa taifa kwa kuwa yataisaidia Serikali na Wizara husika kupata suluhisho la changamoto mbalimbali, ikiwemo uharibifu wa miundombinu unaosababishwa na mabadiliko ya tabianchi.

Alisisitiza kuwa wajibu wa watafiti na wadau wa sekta ya sayansi haupaswi kuishia katika mikutano na machapisho pekee, bali wanapaswa kufuatilia kwa karibu kuhakikisha matokeo ya tafiti yanatumika ipasavyo kwa manufaa ya wananchi.

“Hatupaswi kuishia kwenye huu mkutano pekee, bali tuwajibike kwa wananchi kwa kuwapatia matokeo ya tafiti na kuelekeza matumizi bora ya matokeo hayo,” alisema Profesa Mushi.

Aliongeza kuwa mabadiliko ya tabianchi ni janga la dunia lenye athari kubwa kwa mataifa yote, ikiwemo Tanzania, na kwamba yanatishia tija ya kilimo ambacho ni uti wa mgongo wa uchumi wa nchi. Pia alisema mabadiliko ya tabianchi huongeza gharama za kukabiliana na majanga na ukarabati wa miundombinu, hali inayopunguza rasilimali ambazo zingeweza kuwekeza katika sekta za elimu, afya na vipaumbele vingine vya maendeleo.

Kwa mujibu wake, kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi kunahitaji utafiti wa kina ili kuboresha sera na mikakati ya Serikali. Alisisitiza kuwa utafiti wa mabadiliko ya tabianchi usilenge tu kuongeza maarifa ya kitaaluma, bali uzingatie zaidi kutatua matatizo halisi yanayolikabili taifa.

Alibainisha kuwa Serikali inatambua umuhimu wa utafiti katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, ndiyo maana ilianzisha Programu ya Utafiti wa Mabadiliko ya Tabianchi inayoratibiwa na COSTECH.

Profesa Mushi alisema utekelezaji wa programu hiyo unahusisha Vyuo Vikuu na taasisi za utafiti 20 nchini, ikiwa ni sehemu ya uwekezaji wa Serikali unaolenga kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi katika sekta mbalimbali.

Alisema hadi sasa programu hiyo imepatiwa jumla ya Sh bilioni 14.5, ambapo Sh bilioni 12.1 tayari zimewekezwa katika miradi 39 ya utafiti inayojikita kuchunguza na kutafuta suluhisho la changamoto za mabadiliko ya tabianchi katika sekta za kilimo, maliasili, afya, nishati, maji pamoja na mifumo ya kijamii na kiuchumi.

Aliongeza kuwa matarajio ya Serikali kwa watafiti waliopata fedha hizo ni makubwa, na kwamba anatarajia miradi 34 kati ya hiyo kuwasilisha matokeo ya tafiti zao katika mkutano huo.

“Nitoe wito kwa watekelezaji wa miradi yote 39 kuhakikisha kila shilingi inatumika kwa malengo yaliyokusudiwa. COSTECH ihakikishe inasimamia vyema fedha za utafiti na kuratibu uwasilishaji wa matokeo kwa wadau wote,” alisema.

Katika hatua nyingine, aliwataka watafiti kuhakikisha tafiti zao zinaendana na vipaumbele vya kitaifa, kushirikisha wananchi, watendaji na watunga sera katika hatua zote za utafiti, badala ya kusubiri mwisho wa miradi na kuwasilisha matokeo kupitia machapisho pekee.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa COSTECH, Dkt. Amos Nungu, alisema kuwa hadi sasa programu hiyo imeshirikisha Taasisi 13, Vyuo Vikuu 12 na Mashirika yasiyo ya kiserikali (NGO), huku jumla ya watafiti 200 na wanafunzi 90 wakishiriki.

Dkt. Nungu aliwashukuru wafadhili wa programu hiyo, akiwataja kuwa ni SIDA na Serikali ya Norway, kwa ushirikiano wao mkubwa katika kufanikisha utekelezaji wa programu ya utafiti wa mabadiliko ya tabianchi nchini.

Kwa upande wake mwakilishi wa SIDA Dkt. Johanna Variandek alisema wataendelea kushirikiana na Serikali ili kuhakikisha tafifi mbalimbali zinafanya vizuri.

Mwenyekiti wa Bodi ya Makamishna ya COSTECH Prof. John Kondoro alisema mkutano huo utakuwa na majawabu yenye ushahidi wa kisayansi ambayo yatasaidia kutatua changamoto mbalimbali zitokanazo na athari za mabadiliko ya tabia nchi.










Na Mwandishi wetu - Dodoma

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Daniel Mushi, amesrma matokeo ya tafiti ni muhimu kwa taifa kwa kuwa yataisaidia Serikali na Wizara husika kupata suluhisho la changamoto mbalimbali, ikiwemo uharibifu wa miundombinu unaosababishwa na mabadiliko ya tabianchi.

Prof Mushi ameyazungumza hayo leo Jijini Dodoma wakati wa ufunguzi wa mkutano wa kwanza wa kila mwaka wa maendeleo ya utafiti chini ya Programu ya Utafiti wa Mabadiliko ya Tabianchi, ambapo mesema kuwa wajibu wa watafiti na wadau wa Sekta ya sayansi haupaswi kuishia katika mikutano na machapisho pekee, bali wanapaswa kufuatilia kwa karibu kuhakikisha matokeo ya tafiti yanatumika ipasavyo kwa manufaa ya wananchi.

“Hatupaswi kuishia kwenye huu mkutano pekee, bali tuwajibike kwa wananchi kwa kuwapatia matokeo ya tafiti na kuelekeza matumizi bora ya matokeo hayo,"

Ameongeza kuwa matokeo ya tafiti ni muhimu kwa taifa kwa kuwa yataisaidia serikali na wizara husika kupata suluhisho la changamoto mbalimbali, ikiwemo uharibifu wa miundombinu unaosababishwa na mabadiliko ya tabianchi.

Amesema matarajio ya Serikali kwa watafiti waliopata fedha hizo ni makubwa, na kwamba anatarajia miradi 34 kati ya hiyo kuwasilisha matokeo ya tafiti zao katika mkutano huo.

Amesema utekelezaji wa programu hiyo unahusisha vyuo vikuu na taasisi za utafiti 20 nchini, ikiwa ni sehemu ya uwekezaji wa serikali unaolenga kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi katika sekta mbalimbali.

Prof. Mushi amesema Kuwa hadi sasa programu hiyo imepatiwa jumla ya Sh bilioni 14.5, ambapo Sh bilioni 12.1 tayari zimewekezwa katika miradi 39 ya utafiti inayojikita kuchunguza na kutafuta suluhisho la changamoto za mabadiliko ya tabianchi katika sekta za kilimo, maliasili, afya, nishati, maji pamoja na mifumo ya kijamii na kiuchumi.

“Nitoe wito kwa watekelezaji wa miradi yote 39 kuhakikisha kila shilingi inatumika kwa malengo yaliyokusudiwa. COSTECH ihakikishe inasimamia vyema fedha za utafiti na kuratibu uwasilishaji wa matokeo kwa wadau wote,” alisema.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa COSTECH, Dkt Amos Nungu, alisema kuwa hadi sasa programu hiyo imeshirikisha taasisi 13, vyuo vikuu 12 na mashirika yasiyo ya kiserikali (NGO), huku jumla ya watafiti 200 na wanafunzi 90 wakishiriki.

Dkt Nungu aliwashukuru wafadhili wa programu hiyo, akiwataja kuwa ni SIDA na Serikali ya Norway, kwa ushirikiano wao mkubwa katika kufanikisha utekelezaji wa programu ya utafiti wa mabadiliko ya tabianchi nchini.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Makamishna COSTECH Profesa John Kandoro alisema mkutano huo utakuwa na majawabu yenye ushahidi wa kisayansi ambayo yatasaidia kutatua changamoto mbalimbali zitokanazo na athari za mabadiliko ya tabia nchi.

Kwa upande wake mwakilishi wa SIDA DK Johanna Variandek alisema wataendea kushirikiana na serikali ili kuhakikisha tafifi mbalimbali zinafanya vizuri.





Maafisa,na askari wa vyeo mbalimbali kutoka Jeshi la Polisi Nchini Tanzania ambao nikundi lilomaliza muda wake wa kuhudum kulinda amani nchini Sudan kusini wamehitimisha kwa Paredi maalum ambayo ili ambatana na kuwavisha nishani( Medall Pin) maafisa na askari hao ikiwatambua kwa kazi nzuri ya kudumisha amani.

Tanzania ni miongoni mwa nchi bora zinazochangia askari wake katika Operesheni za kulinda amani za Umoja wa Mataifa.

Aidha Miongoni mwa maafisa hao wamebainisha kuwa licha ya kuwa mazingira magumu ya iliwapa moyo kuendelea kulinda amani na kutoa elimu kwa makundi mengi zaidi.

Sambamba na hilo wameendelea kuwashukuru maafisa wengine wa majeshi kwa namna walivyoshirikiana kudumisha amani katika misheni ya kulinda amani nchini Sudan Kusini

Mwisho wamewaomba wananchi wa Sudan kusini kuendelea kutunza na kulinda amani ya nchini hiyo.
















-Ni utekelezaji wa ahadi za Rais Dkt. Samia ndani ya siku 100 tangu achaguliwe
 
WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amekabidhi hundi ya shilingi bilioni 200 kwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Maendeleo ya Vijana, Joel Nanauka ikiwa ni utekelezaji wa vitendo wa ahadi ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan aliyoitoa wakati wa Kampeni za Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025, ya kutenga na kutoa mitaji kwa ajili ya kuwawezesha vijana na wanawake.
 
Pia, Waziri Mkuu amesema uwezeshaji wananchi kiuchumi ni mhimili wa kukuza uzalishaji, biashara, uwekezaji na ustawi wa maisha ya wananchi, hasa vijana na wanawake ambapo amezitaka wizara, taasisi na mamlaka za kisekta zinazoendelea kutekeleza mpango huo kuhakikisha fedha hizo zinawafikia walengwa wote na program zilizokusudiwa na kutoa tija tarajiwa.
 
“Utoaji wa Hundi ya Shilingi Bilioni 200 unaonesha kwa vitendo kwamba Serikali ya Awamu ya Sita inatekeleza ahadi zake kwa vitendo, si kwa maneno. Tukio hili linaweka msingi mpya wa kuimarisha ushiriki wa vijana na wanawake katika uchumi wa Taifa na kuharakisha safari ya Tanzania kuelekea uchumi jumuishi na endelevu.”
 
Amekabidhi hundi hiyo leo Alhamisi, Februari 5, 2026 katika ukumbi wa Mikutano wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Mlimwa jijini Dodoma, ambapo pamoja na mambo mengine amesisitiza kuwa mafanikio hayo hayatapimwa kwa kiasi cha fedha kilichotolewa, bali kwa mabadiliko halisi ya maisha ya wananchi, hususan vijana na wanawake.
 
“Wizara, Taasisi na Mamlaka zote zinazoshiriki katika utekelezaji wa uwezeshaji kiuchumi lazima zibadilishe mtazamo kutoka katika kutoa fedha kwenda katika kusimamia matokeo na kwamba kila taasisi ijiwekee malengo yanayopimika, viashiria vya utendaji na ratiba za utekelezaji, ili kuhakikisha mitaji hiyo inazalisha ajira, kipato na biashara endelevu.”

Waziri Mkuu amesisitiza kwamba uwezeshaji huo usiwe zoezi la kawaida la kiofisi bali uwe chombo cha mageuzi ya kiuchumi, hivyo utekelezaji wa Shilingi Bilioni 200 lazima uendeshwe kwa uwazi na uwajibikaji. “Taarifa za maendeleo zitolewe mara kwa mara, na hatua zichukuliwe dhidi ya matumizi mabaya. Serikali haitasita kuchukua hatua kwa yeyote atakayekiuka dhamira ya uwezeshaji huu.”

Kadhalika, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu amesema katika kipindi kifupi cha Novemba 2024 hadi Januari 2025, Serikali kupitia mifuko na programu za kuwawezesha wananchi kuichumi imetoa mikopo na dhamana zenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 66.9 kwa wanufaika zaidi ya 13,000, wakiwemo vijana na wanawake katika sekta mbalimbali.

Kwa upande wake, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu); William Lukuvi amemshukuru Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuwa kinara katika kukuza uwezeshaji kiuchumi pamoja na jitihada mbalimbali anazofanya katika kuhakikisha vijana na wanawake wanashiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi ikiwa ni pamoja na kuwawezesha mitaji.

Waziri Lukuvi amesema hata hivyo, changamoto ya upatikanaji wa mitaji ikiwemo mikopo, vifaa, mashine na mitambo bado imekuwa kikwazo kikubwa cha ukuaji wa shughuli za kiuchumi zinazotekelezwa na vijana na wanawake. ”Kutokana na changamoto hiyo, Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameongeza fedha shilingi bilioni 200 kwa ajili ya kuwawezesha vijana na wanawake.
 
Amesema uwezeshaji huo wa shilingi bilioni 200 ni uthibitisho wa maono na dhamira aliyonayo Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan inayolenga kupanua wigo wa upatikanaji wa mitaji ya gharama nafuu kwa vijana na wanawake ili waweze kuwa shindani kitaifa, kikanda na kimataifa.


Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba akimkabidhi Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Maendeleo ya Vijana Mhe. Joel Nanauka, hundi ya shilingi bilioni 200 ambazo ni ahadi ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa ajili ya mitaji ya kuwawezesha vijana na wanawake, hafla hiyo imefanyika katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Mlimwa jijini Dodoma, Februari 05, 2026. kulia  ni kutoka kwa Waziri wa Fedha Balozi Khamis Mussa Omar na kushoto ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) William Lukuvi.
Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba akipokea kutoka kwa Waziri wa Fedha Balozi Khamis Mussa Omar hundi ya shilingi bilioni 200 ambazo ni ahadi ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa ajili ya mitaji ya kuwawezesha vijana na wanawake, hafla hiyo imefanyika katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Mlimwa jijini Dodoma, Februari 05, 2026.




 


Top News