Na Janeth Raphael - MichuziTv
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, amewataka wananchi wanaomiliki silaha kuhakikisha wanakamilisha taratibu zote za kisheria na vibali vinavyohitajika kabla ya Agosti 30, 2026, akieleza kuwa operesheni maalum ya ukaguzi wa silaha itaanza mara baada ya muda huo.
Chalamila ametoa agizo hilo wakati akizungumza na waandishi wa habari leo , akisisitiza kuwa wamiliki ambao kwa sababu mbalimbali, ikiwemo kusahau au kutokuwa na uelewa wa kutosha kuhusu taratibu, hawajakamilisha malipo ya vibali au hatua nyingine za kisheria, wanapaswa kutumia muda uliopo kufika katika mamlaka husika na kurekebisha hali hiyo.
Amesema hatua hiyo inalenga kuhakikisha silaha zinazomilikiwa na wananchi katika Mkoa wa Dar es Salaam zinakuwa na kumbukumbu na vibali halali vinavyotambulika kisheria, kabla ya kuanza kwa operesheni hiyo.
Kwa upande mwingine, Mkuu huyo wa Mkoa amewataka watu wanaomiliki silaha bila kufuata sheria kuzisalimisha kwa hiari katika Jeshi la Polisi au kituo cha Polisi kilicho karibu kabla ya operesheni kuanza. Amesisitiza kuwa hatua hiyo inaweza kusaidia wahusika kuepuka kukumbana na hatua za kisheria zitakazochukuliwa baada ya ukaguzi kuanza.
Aidha, Chalamila ametoa mwito kwa familia ambazo ndugu zao wamefariki huku wakiacha silaha zenye vibali halali kuhakikisha hazizifichi wala kuzihamisha bila kufuata utaratibu. Badala yake, amewataka kuwasilisha taarifa pamoja na silaha hizo kwa mamlaka husika ili kupata maelekezo ya kisheria kuhusu namna ya kushughulikia umiliki huo.
Kuhusu silaha zinazoripotiwa kuibiwa, amewataka wamiliki kutoa taarifa Polisi na kufuata taratibu zote zinazohitajika. Amesisitiza kuwa silaha hizo zinapopatikana, wahusika hawapaswi kuzificha au kuendelea kuzitumia bila kufuata maelekezo ya mamlaka.
Chalamila amesisitiza kuwa Agosti 30, 2026 ndiyo mwisho wa muda uliotolewa kwa wamiliki kuhakikisha wanakamilisha taratibu zao, akieleza kuwa baada ya tarehe hiyo operesheni maalum ya ukaguzi itaanza na yeyote atakayebainika kumiliki silaha kinyume cha sheria atachukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria.
Amewataka wananchi kutotumia muda uliobaki kupuuza agizo hilo, bali kuhakikisha mapema kuwa umiliki wa silaha zao uko katika hali halali na unaotambulika na mamlaka, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha udhibiti na usalama wa silaha katika Mkoa wa Dar es Salaam.

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, amewapa muda wa wiki moja wamiliki na waendeshaji wa kampuni za mabasi makubwa ya mikoani kuhakikisha wanaanza kutumia Stendi ya Magufuli kama kituo cha kuanzia na kumalizia safari zao, katika hatua inayolenga kupunguza msongamano wa magari katikati ya Jiji la Dar es Salaam.
Chalamila ametoa agizo hilo leo jijini Dar es katika Mkutano na waandishi wa habari ambapo amesema mabasi hayo hayatapaswa tena kuingia katikati ya jiji kwa ajili ya kupakia na kushusha abiria, isipokuwa kampuni sita ambazo tayari zimepewa vibali maalum vya kushusha abiria katika maeneo ya katikati ya jiji.
Chalamila amesema wamiliki na waendeshaji wa mabasi hayo wametakiwa kutumia muda uliopo hadi Agosti 17, 2026 kufanya maandalizi muhimu, huku utekelezaji wa agizo hilo ukianza rasmi baada ya tarehe hiyo.
Ameeleza kuwa mabasi makubwa yanapoingia katikati ya jiji kwa ajili ya kushusha au kupakia abiria, yanaongeza idadi ya magari katika maeneo ambayo tayari yana msongamano mkubwa, hivyo matumizi ya Stendi ya Magufuli yatasaidia kuyapunguza mabasi hayo katika maeneo ya katikati ya jiji na kuweka utaratibu mzuri wa usafirishaji wa abiria wanaoingia au kutoka Dar es Salaam.
Chalamila amesema abiria watakaofikishwa katika Stendi ya Magufuli hawataachwa bila usafiri wa kuendelea na safari zao, kwani wataweza kutumia huduma mbalimbali za usafiri wa ndani kuelekea maeneo wanayokwenda.
Kwa mujibu wa Chalamila, utaratibu huo hautalenga tu kupunguza msongamano wa magari, bali pia unalenga kulinda na kuongeza fursa za ajira na biashara kwa waendeshaji wa usafiri wa ndani.
Amesema mfumo huo mpya utawezesha kuwepo kwa mgawanyo mzuri wa majukumu katika sekta ya usafirishaji, ambapo mabasi makubwa yatabeba abiria kutoka mikoa mbalimbali na kuwafikisha katika Stendi ya Magufuli, kisha usafiri wa ndani kuchukua jukumu la kuwaunganisha abiria hao na maeneo mbalimbali ndani ya Dar es Salaam.
Chalamila amewataka wamiliki na waendeshaji wa mabasi makubwa kutumia muda uliotolewa kufanya maandalizi ya kutosha, ikiwemo kupanga namna ya kuwasaidia abiria wao kuendelea na safari kutoka Stendi ya Magufuli.
Hatua hiyo inatarajiwa kuwa sehemu ya mabadiliko katika mfumo wa usafiri wa Mabasi ya masafa marefu jijini Dar es Salaam, huku Serikali ikilenga kuhakikisha mabasi makubwa yanafanya shughuli zake katika vituo vilivyotengwa na abiria wanapata huduma rahisi na salama za usafiri wa ndani kuelekea wanakokwenda.
FARIDA SAID, MOROGORO
Ng'ombe 56 waliokuwa mali ya mfugaji Clement Bernad sasa wamebaki kuwa sehemu ya historia yake ya ufugaji, ukame unaochochewa na mabadiliko ya tabianchi na kupungua kwa malisho vimemlazimisha kubadili mfumo wa ufugaji, akipunguza idadi ya mifugo na kuanza kuangalia zaidi uwezo wa kuzalisha malisho na kuihudumia mifugo aliyonayo.
Bernad mkazi wa kijiji cha Mtanana wilayani Kongwa Mkoa wa Dodoma ni mfano wa mabadiliko yanayowakabili wafugaji katika eneo hilo, uhaba wa malisho unalazimisha mifugo kutafuta chakula nje ya maeneo ya wafugaji na wakati mwingine kuingia katika mashamba ya wakulima, hali inayochochea migogoro kati ya pande hizo mbili.
Bernad anasema baada ya kupata elimu kutoka kwa wataalam kutoka Chuo kikuu cha Sokoine cha kilimo ( SUA ) kuhusu ufugaji unaozingatia mabadiliko ya tabianchi, ameamua kupunguza idadi ya ng'ombe wake na kubaki na idadi anayoamini anaweza kuihudumia kwa malisho na rasilimali alizonazo.
"Nilikuwa na ng'ombe 56 wa kienyeji, lakini baada ya kupata elimu nimeona umuhimu wa kuwa na mifugo ambayo ninaweza kuihudumia vizuri badala ya kuwa na mifugo mingi ambayo inakosa chakula," anasema Bernad.
Uamuzi huo unaakisi changamoto kubwa inayowakabili wafugaji nchini ambapo mabadiliko ya tabianchi yamekuwa yakibadilisha upatikanaji wa malisho na maji, hali inayogusa moja kwa moja uzalishaji wa mifugo ikiwemo maziwa.
Afisa Ugani wa Kata ya Mtanana Dominica Samweli Swai, anasema mabadiliko ya tabianchi yamekuwa miongoni mwa sababu zinazoendelea kuchochea migogoro kati ya wakulima na wafugaji kwasababau wafugaji wakikosa malisho wanalazimika kuuingiza mifugo kwenye mashamba ya wakulima.
Anasema suluhisho mojawapo ni kuwahamasisha wafugaji kuanza kuzalisha malisho katika maeneo yao ili kupunguza utegemezi wa malisho ya asili na ulazima wa kupeleka mifugo kutafuta chakula maeneo mengine.
"Wafugaji wengi wamehamasika kupanda malisho katika maeneo yao. Kama wafugaji watabadilika na kuacha mfumo wa kuchunga mifugo yao bila kuwa na uhakika wa malisho, tunaweza kupunguza migogoro mingi kati ya wakulima na wafugaji," anasema Swai.
Kata ya Mtanana pekee wafugaji 1,320 wenye jumla ya mifugo 7,829, idadi inayoweka wazi ukubwa wa mahitaji ya malisho katika eneo ambalo linakabiliwa na changamoto ya ukame.
Hata hivyo, kupanda malisho pekee kunaweza kusiwe jibu la muda mrefu iwapo aina ya malisho inayotumika haiwezi kustahimili vipindi virefu vya ukame.
Hapo ndipo watafiti kutoka Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) wameingia kazini kutafuta aina za malisho zinazoweza kustahimili ukame, huku wakilenga kutoa suluhisho linaloweza kuwasaidia wafugaji kuendelea kuzalisha mifugo hata katika mazingira yanayobadilika kutokana na mabadiliko ya tabianchi.
Akizungmza na waandishi wa habari Mkuu wa mradi kutoka Idara ya sayansi za wanyama, ufugaji viumbe maji na nyanda za malisho Chuo kikuu SUA, Prof. Sebastian Chenyambaga amesema utafiti huo ni sehemu ya mradi unaolenga kuimarisha uwezo wa wafugaji kustahimili na kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi, unaofadhiliwa na Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH).
Mradi huo wa miaka mitatu ulianza Oktoba 2025 na unatarajiwa kukamilika mwaka 2028, ukiangalia namna mabadiliko ya tabianchi yanavyowaathiri wafugaji na kutafuta mbinu zinazoweza kuongeza uwezo wao wa kukabiliana na athari hizo.
Mradi unatekelezwa katika Wilaya ya Kongwa mkoani Dodoma, Kishapu mkoani Shinyanga na Miatu mkoani Simiyu, maeneo ambayo yamechaguliwa katika utekelezaji wa utafiti huo.
Kwa upande wake Mtafiti kutoka Idara ya sayansi za wanyama, ufugaji viumbe maji na nyanda za malisho Chuo kikuu SUA, Dkt. Doris Lutatenekwa amesema utafiti pia unaenda sambamba na kupima aina za malisho zinazostahimili ukame.
Lengo la utafiti huo si kutafuta malisho ya kuokoa mifugo pekee, bali pia kuangalia namna wafugaji wanavyoweza kuendelea kuzalisha maziwa na bidhaa nyingine za mifugo katika mazingira yenye changamoto ya ukame.
Mkurugenzi wa Costech Dkt. Amos Nungu anasema mradi huo ni miongoni mwa hatua zinazolenga kutekeleza Dira ya Tanzania ya 2050 kwa kutumia sayansi, teknolojia na ubunifu katika kutatua changamoto zinazoikabili jamii.
Anasema tafiti zinazolenga kupata suluhisho la changamoto za mabadiliko ya tabianchi ni muhimu katika kujenga jamii yenye uwezo wa kustahimili mabadiliko ya mazingira na kulinda shughuli za kiuchumi za wananchi.
Kwa wafugaji kama Bernad, mabadiliko hayo hayapo tena kwenye vitabu au mijadala ya wataalamu, yameingia moja kwa moja katika maisha yao yakimlazimisha mfugaji kujiuliza si tu “nitafuga ng'ombe wangapi?”, bali pia “nitawapataje chakula wakati mvua hazitoshelezi?”
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, akizungumza na viongozi wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), Ikulu Chamwino, mkoani Dodoma, tarehe 10 Agosti, 2026.
Katibu NEC Itikadi, Uenezi na Mafunzo, Ndugu Kenani Kihongosi amesisitiza kuwa Vijana ndio walinda Nchi hivyo wanatakiwa kuilinda amani ya nchi ili waweze kufanya shughuli za uzalishaji kwa maendeleo ya Taifa na familia zao.
Ndugu Kenani ameyasema hayo leo tarehe 10 Agosti 2026 wakati akitoa mada kwenye Mafunzo ya Uongozi wa Seneti za Vyuo vya Kati na Vyuo Vikuu yanayofanyika katika Chuo cha Mafunzo Ihemi mkoani Iringa.
Pia, ametumia jukwaa hilo kukemea lugha chafu zinazotolewa kwa Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan katika mitandao ya kijamii na kuwasihi vijana kuwa mstari wa mbele kumtetea Rais na wasikae kimya.
Aidha ametoa wito kwa Vijana wa Chama cha Mapinduzi ndani na nje ya Tanzania kulipa Ada ya uanachama akieleza uhai wa Chama cha Mapinduzi (CCM) unatokana na wanachama kulipia ada.
Mwenyekiti wa Jumuiya ya wawake (UWT) Wilaya ya Kibahaa mjini Elina Mgonja Katika kuuunga juhudi za Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuwakomboa wanawake kiuchumi ameamua kutoa mafunzo ya ujasiriamali kwa vitendo kwa wanawake wapatao 400 wa Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha Mkoa wa Pwani kwa lengo la kuondokana na wimbi la umasikini.
Akizungumza katika ziara yake maaalumu ya kikazi yenye lengo la kuwatembelea wanawake wa (UWT) katika kata mbali mbali kwa ajili ya kuwapa maarifa na ujuzi na kujifunza jinsi ya kutengeneza bidhaa za aina tofauti ambazo zitawapa fursa ya kujiajiri wao wenyewe na kuondokana na kuwa tegemezi kila kukicha.
Elina amebainisha kuwa amefanya ziara hiyo ikiwa ni utekelezaji wa ahadi yake ambayo aliitoa ya kuwasaidia wanawake wa UWT kutoka kata zote 14 zilizopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha na kwamba mafunzo hayo ambayo ameamua kuyatoa bure bila malipo yoyote yatakuwa ni mkombozi mkubwa katika kujikwamua kiuchumi,
Nao baadhi ya wanawake ambao wamepata mafunzo hayo akiwemo Mwajuma Makuka wamesema kwamba maffunnzo hayo yataweza kuwasaidia kwa kiasi kikubwa kuondokana na kuwa tegemezi na kwamba watakwenda kuyafanyia kazi kwa hali na mali kwa lengo la kuweza kuondokana na wimbi la umasikini.
"Kwa kweli tunapenda kumshukuru kwa dhati Mwenyekiti wetu wa UWT Wilaya ya Kibaha mjini Elina Mgonjwa kwa kuweza kufanya ziara hii na kuja kutupa elimu na mafunzo ya ujasiliamali na tumeweza kujifunza mambo mbali mbali ikiwemo kutengeneza bidhaa kama vile kutengeneza batiki, sabuni za kufulia, sabuni za kuogea pamoja na kupata ujuzi ambao tutakwenda kuufanyia kazi katika kutekeleza majukumu yetu,"amebainisha Mwajuma.
Mwenyekiti huyo wa UWT anaendelea na ziara yake ya kikazi ambapo hadi sasa ameshatembelea kata 7 ambazo ni Msangani, Mkuza, Tumbi, Maili moja, Kongowe, Kibaha pamoja na Kata ya Misususugu ambapo jumla ya wanawake 400 wameweza kunufaika na mafunzo hayo ya ujasiriamali kwa vitendo.
Wizara ya Fedha kwa kushirikiana na Taasisi ya Saratani Ocean Road imeanza kutekeleza zoezi la utoaji wa elimu kuhusu saratani pamoja na vipimo vya uchunguzi wa awali wa saratani kwa watumishi wa Wizara hiyo ili kuongeza uelewa wa namna ya kujikinga, kutambua dalili za awali na kuchukua hatua stahiki kukabiliana na ugonjwa huo.
Zoezi hilo litakalohusisha utoaji wa elimu kuhusu saratani mbalimbali, ikiwemo saratani ya matiti, tezi dume na shingo ya kizazi, pamoja na vipimo vya awali linatarajiwa kufanyika kuanzia tarehe 10 hadi 14 Agosti 2026, katika Ofisi za Wizara ya Fedha, Mtumba, jijini Dodoma.
Akizungumza wakati akifungua mafunzo hayo, Mkurugenzi wa Usimamizi wa Mali za Serikali, Wizara ya Fedha, Bw. Chotto Sendo, alisema ni muhimu kwa watumishi kufuatilia elimu ya afya ya saratani ili kuwa na uelewa wa kutosha kukabiliana na ugonjwa huo.
‘‘Ni muhimu kuwa na uelewa sahihi kuhusu saratani, hususan kwa kuzingatia kwamba utambuzi wa ugonjwa huo katika hatua za awali una nafasi kubwa katika matibabu na kuokoa maisha’’’ Alisema Bw. Sendo.
Aliwasisitiza watumishi wa Wizara hiyo kutumia fursa hiyo kupata elimu pamoja na kufanya vipimo vya awali vinavyotolewa ili kufahamu hali zao za afya.
Kwa upande wake Daktari Bingwa wa Saratani, Taasisi ya Saratani Ocean Road, Dkt. Frank Ruta, aliwahimiza watumishi hao kutopuuza mabadiliko au dalili zisizo za kawaida katika miili yao na kufika katika vituo vya afya kwa ajili ya uchunguzi na ushauri wa kitaalamu.
Alisema utambuzi wa saratani katika hatua za awali unaongeza nafasi ya mafanikio ya matibabu, hivyo jamii inapaswa kujenga utamaduni wa kufanya uchunguzi wa afya mara kwa mara na kuchukua hatua za mapema katika kuzuia na kukabiliana na saratani.
Dkt. Ruta alisemna elimu hiyo ni sehemu ya jitihada za kuimarisha uelewa wa watumishi na jamii kwa ujumla kuhusu afya na kuwahamasisha kuchukua hatua za mapema katika kuzuia na kukabiliana na saratani.

Mkurugenzi wa Idara ya Usimamizi wa Mali za Serikali, Wizara ya Fedha, Bw. Chotto Sendo, akizungumza katika zoezi la utoaji wa elimu kuhusu saratani pamoja na vipimo vya uchunguzi wa awali wa saratani kwa watumishi wa wizara hiyo, linalofanyika katika Ofisi za Wizara ya Fedha, Mtumba, jijini Dodoma, kuanzia tarehe 10 hadi 14 Agosti 2026.

Afisa Utumishi Mwandamizi, Wizara ya Fedha, Bw. Salum Said, akifafanua jambo katika zoezi la utoaji wa elimu kuhusu saratani pamoja na vipimo vya uchunguzi wa awali wa saratani kwa watumishi wa Wizara hiyo, linalofanyika katika Ofisi za Wizara ya Fedha, Mtumba, jijini Dodoma, kuanzia tarehe 10 hadi 14 Agosti 2026.


Daktari Bingwa wa Saratani kutoka Taasisi ya Saratani Ocean Road, Dkt. Frank Ruta, akitoa elimu kuhusu kinga, utambuzi na matibabu ya saratani kwa watumishi wa Wizara ya Fedha, katika zoezi linalofanyika katika Ofisi za Wizara ya Fedha, Mtumba, jijini Dodoma, kuanzia tarehe 10 hadi 14 Agosti 2026.


Baadhi ya Watumishi wa Wizara ya Fedha wakifuatilia elimu iliyokuwa inatolewa na wataalamu kutoka Taasisi ya Saratani Ocean Road, kuhusu namna ya kujikinga, kutambua dalili za awali na kuchukua hatua stahiki katika kukabiliana na ugonjwa wa saratani, katika zoezi linalofanyika katika Ofisi za Wizara ya Fedha, Mtumba, jijini Dodoma, kuanzia tarehe 10 hadi 14 Agosti 2026.
(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, WF, Dodoma)










.jpeg)






.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)












.jpeg)






.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)

