-Lumbila Wapata Umeme kwa Mara ya Kwanza Tangu Uhuru

-Giza la Miaka 60 Lamalizika Wilayani Ludewa


Ludewa, Njombe📍

Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kwa kushirikiana na mkandarasi; Shirika la Uzalishaji Mali JKT (SUMA JKT) leo, tarehe 25 Juni, 2026 kwa mara ya kwanza wamewasha umeme katika kitongoji cha Lumbila katika Halmashauri ya wilaya ya Ludewa ambapo eneo hilo lilikuwa halijapa umeme tangu Tanzania ipate uhuru wake 9 Desemba, mwaka 1961.

Akiongoza hafla hiyo ya kuwasha umeme kwa mara ya kwanza, Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB); Bodi inayoisimamia REA; Mhe. Balozi na Meja Jenerali Mstaafu, Jacob Kingu alisema utekelezaji wa mradi huo ni ushahidi wa dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha huduma ya umeme inawafikia Watanzania wote bila kujali umbali na changamoto za kijiografia.

Eneo hili lilikuwa halijawahi kupata umeme kwa zaidi ya miaka 60 tangu Tanzania ipate uhuru wake mwaka 1961. Hafla hiyo ya kuwasha umeme kwa mara ya kwanza katika Kitongoji cha Lumbila imefanyika katika Kanisa Katoliki la Kitongoji cha Lumbila, hatua iliyopokelewa kwa furaha kubwa na Wananchi wa eneo hilo.

Awali kabla ya kumkaribisha Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB); Mheshimiwa Balozi na Meja Jenerali Mstaafu, Jacob Kingu, Mhandisi, Thomas Mmbaga amaye alimwakilisha Mkurugenzi wa Umeme Vijijini alisema, Mradi wa kusambaza umeme kwenye vitongoji sita vya mwambao wa Ziwa Nyasa umetumia gharama ya Shilingi bilioni 3.124 na kuongeza kuwa hadi sasa mradi umefikia asilimia 67, ambapo vitongoji 3 kati ya 6 vya mwambao wa Ziwa Nyasa vimeshawashiwa umeme.

Mhandisi Mmbaga ameongeza kuwa Mradi unahusisha ujenzi wa kilomita 36.6 za njia za msongo wa kati na kilomita 15.1 za msongo mdogo.

“Mradi unatarajiwa kuwafikia wateja 151 wa njia moja (single-phase) na wateja 9 wa njia tatu (three-phase). Tayari kaya zaidi ya 23 zimeomba kuunganishiwa”. Amekaririwa, Mhandisi, Mmbaga.

Naye, Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya SUMA JKT Company Ltd, Meja James Simon Mwame, alisema utekelezaji wa Mradi huo ulikuwa na changamoto kubwa kutokana na mazingira ya mwambao wa Ziwa Nyasa, lakini juhudi za wataalam na wafanyakazi wa kampuni hiyo zimewezesha ndoto ya Wananchi kupata umeme kutimia.

Meja Mwame alisema SUMA JKT ni kampuni inayojihusisha na ujenzi na usambazaji wa miundombinu ya umeme nchini, na kwa Mkoa wa Njombe kampuni hiyo inatekeleza miradi ya usambazaji umeme katika wilaya za Ludewa na Makete.

Ziara ya viongozi (ikiongozwa na Mwenyekiti wa Bodi ya REA, Balozi Jacob Kingu) ilihusisha safari ya majini kwa boti ya takribani kilomita 11 kutoka Pwani ya Matema (Kyela, Mbeya) hadi Ludewa kutokana na ugumu wa kijiografia na miundombinu ya usafirishaji wa vifaa.

Mwananchi wa eneo hilo, Bakari Gowele, amebainisha kuwa umeme huo utasaidia sana sekta ya uvuvi kwani sasa wataweza kutengeneza barafu na kuhifadhi samaki kwa muda mrefu ili kuwafikisha kwenye masoko ya mbali wakiwa katika ubora wa hali ya juu.








-Asilimia 80 ya Mizigo Inaingia Tanzania Kwa Njia ya Maji

NA MWANDISHI WETU, KIGOMA

WAZIRI wa Uchukuzi, Profesa Makame Mnyaa Mbarawa, amesema mabaharia ni nguzo muhimu ya usafirishaji duniani na walinzi wakuu wa mnyororo wa biashara na uchumi, hivyo wanapaswa kuendelea kupewa mazingira bora ya kazi, mafunzo na fursa za maendeleo ili kuongeza mchango wao katika uchumi wa taifa.

Profesa Mbarawa ametoa kauli hiyo wakati wa kilele cha Maadhimisho ya 16  Siku ya Mabaharia Duniani yaliyofanyika mkoani Kigoma.

Alisema zaidi ya asilimia 80 ya biashara ya dunia husafirishwa kwa njia ya maji, jambo linalowafanya mabaharia kuwa mhimili muhimu wa uchumi wa kimataifa licha ya kukabiliwa na changamoto mbalimbali wanazokutana nazo ikiwemo kukaa muda mrefu baharini, kutengana na familia zao, mazingira magumu ya kazi na hatari za kiusalama, bado wanaendelea kutekeleza majukumu yao kwa weledi na kujitolea.

“Mabaharia ndio uti wa mgongo wa sekta ya usafirishaji duniani. Kazi yao inahakikisha bidhaa muhimu zinafika kwa wakati na uchumi wa dunia unaendelea kuzunguka. Tunawapongeza kwa moyo wao wa kujitolea na uzalendo,” alisema.

Amesema kauli mbiu ya maadhimisho hayo inapaswa kutekelezwa kwa vitendo kupitia sera madhubuti, utoaji wa mafunzo ya kisasa na kuimarisha ushirikiano wa kimataifa ili kuhakikisha sekta ya usafiri majini inakua sambamba na mahitaji ya dunia ya sasa.

“Mabaharia ni mhimili mkubwa wa uchumi wa dunia. Tunapaswa kuhakikisha wanapatiwa mafunzo yanayoendana na mabadiliko ya teknolojia na mazingira ya kazi ili waweze kukabiliana na kasi ya mabadiliko yanayotokea duniani,” amesema Profesa Mbarawa.

Ameeleza kuwa maadhimisho ya mwaka huu yanaenda sambamba na juhudi za Serikali za kuongeza uwekezaji katika shughuli za usafirishaji na uchumi wa bluu, hatua ambayo imeendelea kufungua fursa nyingi za ajira kwa vijana na wanawake.

Kwa mujibu wa Waziri huyo, ongezeko la ajira katika sekta ya usafiri majini linaendana na malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayolenga kukuza uchumi, kuongeza uzalishaji na kuboresha maisha ya wananchi.

Aidha, amesema Tanzania na Uganda zimeingia katika makubaliano ya ushirikiano wa shughuli za utafutaji na uokoaji majini, huku akieleza kuwa utekelezaji wa sheria na mifumo ya utafutaji na uokoaji utasaidia kuimarisha usalama wa mabaharia, abiria na vyombo vya usafiri majini.

Profesa Mbarawa amewataka mabaharia kuendelea kuwa waadilifu, kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za kazi pamoja na kutoa taarifa kwa mamlaka husika pindi wanapobaini changamoto zinazoweza kuhatarisha usalama wa vyombo na watu.

Amesema maadhimisho hayo yamekuwa jukwaa muhimu la utoaji elimu, kubadilishana uzoefu na kutoa maelekezo yatakayosaidia kukuza sekta ya usafiri wa majini nchini.

Katika hatua nyingine, ameliagiza Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC) kuharakisha utekelezaji wa mikakati ya kuwatafutia mabaharia wa Tanzania fursa zaidi za ajira katika soko la kimataifa, huku akisisitiza umuhimu wa kuwapa wanawake kipaumbele katika ajira za sekta hiyo.

Pia ameitaka TASAC kukamilisha kanzidata ya mabaharia nchini pamoja na kufanya tathmini ya mifumo ya maslahi yao ili kuhakikisha ustawi wa mabaharia unaimarishwa na changamoto zao zinapatiwa ufumbuzi kwa wakati.

Vilevile, ameshauri TASAC kuendelea kufanya mazungumzo na wamiliki wa meli mbalimbali ili waweze kufungua ofisi zao nchini Tanzania hatua itakayorahisisha upatikanaji wa ajira kwa mabaharia wa Kitanzania na kuongeza ushindani wao katika soko la kimataifa.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa TASAC Mohamed Salum amesema kuwa TASAC imesaini mikataba mbalimbali ya Kimataifa hatua ambayo itasaidia kuongeza uwigo wa ajira kwa mabaharia.

Amesema kuwa Serikali imefanya uwekazaji katika bandari ambapo fursa zimeongezeka kwa mabaharia pamoja kuendelea kuratibu katika mfumo kwa mabaharia kuwa kwenye mfumo huo.

Aidha amesongeza kuwa TASAC imenunua Boti za uokozi ili kuhakikisha wananchi na mabaharia wanakuwa salama wakati wote na wakipata majanga wanaokolewa.

Waziri wa Uchukuzi Profesa Makame Mnyaa Mbarawa (MB)akifunga maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani   yaliyofanyika Viwanja vya Center mjini Kigoma
Mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa ,Mkuu wa Wilaya ya Kigoma Dkt.Rashid Chuachua akizungumza wakati wa kumkaribisha mgeni rasmi katika Kilele cha maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani   yaliyofanyika Viwanja vya Center mjini Kigoma.
Mwenyekiti wa Bodi ya TASAC Nah.Mussa Mandia akitoa maelezo katika kilele cha  maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani   yaliyofanyika Viwanja vya Center mjini Kigoma.
Mkurugenzi Mkuu wa TASAC Mohamed Salum akitoa maelezo kuhusiana na umhimu wa mabaharia  katika maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani   yaliyofanyika Viwanja vya Center mjini Kigoma.
Mkuu wa Chuo cha DMI Profesa Tumain Gurumo akizungumza katika kilele cha maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani   yaliyofanyika Viwanja vya Center mjini Kigoma.


Picha za makundi mbalimbali katika kilele katika maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani   yaliyofanyika Viwanja vya Center mjini Kigoma.


Timu ya wataalamu kutoka Ofisi ya Rais–UTUMISHI kwa kushirikiana na Watumishi Housing Investment imefanya ziara ya ukaguzi wa miradi ya ujenzi wa nyumba za watumishi awamu ya pili katika Wilaya ya Dodoma, ikiwa ni sehemu ya kuhakikisha miradi hiyo inatekelezwa kwa kuzingatia ubora, thamani ya fedha na ratiba iliyopangwa.

Ziara hiyo imeongozwa na Mkurugenzi wa Kitengo cha Ufuatiliaji na Tathmini, Bw. Patrick Allute, ambaye amesema Serikali imeendelea kuimarisha mazingira ya kazi na makazi ya watumishi wa umma ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma kwa wananchi.

Bw. Allute amesisitiza umuhimu wa usimamizi madhubuti wa miradi, matumizi sahihi ya rasilimali za umma na ukamilishaji wa kazi kwa wakati huku viwango vya ubora vikizingatiwa. Aidha, ametoa maelekezo kwa wasimamizi wa miradi na wakandarasi kushughulikia kwa haraka changamoto zilizobainika ili kuhakikisha malengo ya miradi hiyo yanafikiwa kama ilivyopangwa.

Ziara hiyo imekuwa sehemu ya juhudi za Serikali za kuimarisha ufuatiliaji wa miradi ya maendeleo ili kuhakikisha uwekezaji unaofanywa unaleta matokeo yaliyokusudiwa kwa manufaa ya watumishi wa umma na wananchi kwa ujumla.

Katika ukaguzi huo, timu imetembelea miradi ya ujenzi wa nyumba za watumishi katika Kituo cha Afya Hombolo, Shule ya Sekondari Mtemichiloloma, Kituo cha Afya Mkonze na Shule ya Sekondari Bihawana, ambapo imejionea maendeleo ya utekelezaji wa miradi hiyo na imefanya majadiliano na wasimamizi pamoja na wakandarasi kuhusu hatua zilizofikiwa na changamoto zinazojitokeza.



Balozi Mobhare Matinyi akimwonesha Afisa Mtendaji Mkuu wa kampuni ya Géant Electronics, Abdelkrim Mebarkia, vivutio vya utalii na fursa za uwekezaji nchini Tanzania kwenye banda la Tanzania katika Maonesho ya 57 ya Biashara ya Kimataifa ya Algiers (FIA) yanayoendelea nchini Algeria.

Balozi Mobhare Matinyi akipata maelezo ya kitaalam kuhusu uzalishaji wa nyasi bandia zinazotambuliwa na FIFA kutoka kwa Mkurugenzi wa Mauzo na Masoko wa kampuni ya Tapidor ya Algeria, Yahia Ballalou (kulia). Kushoto ni Bounouare Adel, Mkurugenzi wa Uhusiano wa Kimataifa wa Tapidor.
Balozi Mobhare Matinyi akizungumza na washiriki wa taasisi za Serikali ya Tanzania, Robert Mtendawema (kushoto) ambaye ni Meneja wa Tehama na Takwimu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea Tanzania (TFRA), Gilbert Lyimo (wa pili kulia) ambaye ni Kaimu Mhasibu Mkuu wa Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) na Omary Mafita (kulia), Afisa Hesabu Mkuu wa WRRB.


Kampuni za Algeria zinazojishughulisha na uzalishaji wa bidhaa mbalimbali zikiwemo za viwandani na kilimo zinatafuta wabia wa kufanya nazo biashara ya mazao na uwekezaji katika sekta ya viwanda nchini Tanzania.

Kampuni hizo zilizovutiwa kushirikiana na Tanzania zinashiriki katika Maonesho ya 57 ya Biashara ya Kimataifa ya Algiers (FIA) yaliyofunguliwa na Rais Abdelmadjid Tebboune wa Algeria mnamo tarehe 22 Juni, 2026, katika Kituo cha Maonesho cha Shirika la Maonesho na Biashara ya Nje la Algeria (SAFEX).

Maonesho haya ndiyo makubwa zaidi miongoni mwa maonesho ya kimataifa nchini Algeria yakiwa yanazishirikisha jumla ya kampuni 731 zinazojumuisha 549 za Algeria kutoka katika kila sekta na kampuni za kigeni 202 kutoka nchi 36 zikiwemo 16 za Afrika.

Akizungumza katika siku ya pili ya maonesho kwenye banda la Tanzania, Balozi Mobhare Matinyi alizitaja kampuni hizo zinazotafuta wabia nchini kuwa ni GISB inayotaka kuuza vifaa vya umeme na kutengeneza nyaya za umeme kwa kutumia shaba ya Tanzania na GETEX inayotaka kununua katani na pamba na kuwekeza katika kiwanda cha kutengeneza bidhaa za ngozi.

“Afisa Mtendaji Mkuu wa GISB, Dkt. Mohamed Khelifa, anakuja tena nchini mwezi Julai baada ya ziara yake ya kwanza mwezi Mei 2026 wakati watendaji wakuu wa kampuni tatu tanzu za GETEX wamepanga kuja nchini mwezi Oktoba 2026 kutembelea Kiwanda cha Kimataifa cha Bidhaa za Ngozi cha Kilimanjaro (KLICL) ili kuona namna ya kushirikiana”, alisema Balozi Matinyi.

Kampuni zingine ni Tapidor inayotengeneza na kuuza mazulia pamoja na nyasi bandia za viwanja vya soka, Optimaflex ya magodoro, Géant Electronics ya bidhaa za umeme, Bellat ya kusindika nyama na ujenzi wa makaazi pamoja na SARL CPC inayotaka kununua dagaa wa baharini na samaki aina ya jodari ambayo Meneja Mkuu wake, Samir Benhamada, ataitembelea Kampuni ya Uvuvi Zanzibar (ZAFICO) mwezi Julai 2026.

Balozi Matinyi aliongeza zaidi kuwa: “Kampuni zingine za Algeria zinataka kununua bidhaa za kahawa, korosho, ndizi, maharage ya soya, mchele, maziwa ya unga na nyama za ng’ombe, mbuzi na kondoo ambazo huliwa kwa wingi nchini Algeria,” akitolea mfano wa sikukuu ya Idi Al-Adha ambapo Serikali ya Algeria iliingiza kondoo milioni moja kutoka nje ya nchi.

Katika maonesho haya Tanzania inatangaza fahari yake ya utalii wa hifadhi, fukwe za bahari, milima, historia ya kale na utamaduni pamoja na fursa za uwekezaji katika sekta za madini, viwanda, kilimo, nishati na usafirishaji na vilevile mazao ya chakula na biashara.

Mbali ya Ubalozi, taasisi mbili za Serikali ya Tanzania zinazoshiriki ni Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea Tanzania (TFRA) inayowakilishwa na Meneja wa Tehama na Takwimu, Robert Mtendawema; na Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) inayowakilishwa na Kaimu Mhasibu Mkuu Gilbert Lyimo na Afisa Hesabu Mkuu Omary Mafita.

Imetolewa na Ubalozi wa Tanzania,

Algiers, Juni 24, 2026.


Na Karama Kenyunko Michuzi Tv
SERIKALI ya Tanzania imesema iko tayari kuongeza uzalishaji wa bidhaa na kutumia fursa ya soko la China kufuatia hatua ya taifa hilo kuondoa ushuru kwa bidhaa zinazotoka nchi za Afrika.

Balozi wa Tanzania nchini China, Dkt. Suleiman Haji Suleiman, amesema hayo leo Juni 25,2026 jijini Dar es Salaam wakati akizungungumza na waandishi wa habari kuhusu ushirikiano wa Tanzania na China ulipofikia na fursa mbali mbali zitokanazo na ushirikiano huo.

Amesema hatua hiyo inaipa Tanzania nafasi ya kuuza zaidi bidhaa zake katika soko la China bila kutozwa ushuru, mradi bidhaa hizo zikidhi sheria za biashara za China na zile za Jumuiya ya Umoja wa Mataifa.

Akizungumzia mwenendo wa biashara kati ya Tanzania na China, Balozi Suleiman alisema kati ya mwaka 2021 na 2025 thamani ya biashara kati ya nchi hizo mbili imefikia Dola za Marekani bilioni 23.2.

Alisema kati ya kiasi hicho, Tanzania iliuza bidhaa zenye thamani ya Dola za Marekani bilioni 1.8 pekee, sawa na asilimia nane, huku bidhaa zilizoagizwa kutoka China zikifikia Dola za Marekani bilioni 21.3.

Alieleza kuwa pengo hilo linasababishwa na uzalishaji mdogo pamoja na kuendelea kuuza bidhaa ghafi bila kuziongezea thamani kabla ya kuzipeleka katika masoko ya kimataifa.

“Kwa mfano tunapeleka korosho ghafi China, wao wanazifungasha vizuri na kuziongezea thamani, kisha bidhaa hizo zinarejea tena sokoni. Kuna haja ya sisi kuongeza thamani bidhaa zetu hapa nchini kabla ya kuzipeleka nje,” alisema.

Balozi Suleiman alisema ubalozi unaendelea kutafuta fursa zaidi za uwekezaji kutoka China, hususan katika sekta za teknolojia, viwanda na upatikanaji wa mitambo ya kisasa ya uzalishaji ili kusaidia azma ya serikali ya kukuza uchumi wa viwanda.

Alisema makampuni mbalimbali kutoka China tayari yameonesha nia ya kuwekeza nchini, hatua ambayo inatarajiwa kuongeza ajira kwa Watanzania na kukuza uzalishaji wa ndani.

Wakati huo huo, Ubalozi wa Tanzania nchini China umetangaza kufungua kliniki maalumu ya biashara katika Maonesho ya 49 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba) kwa lengo la kutoa ushauri wa moja kwa moja kwa Watanzania wanaotaka kuuza bidhaa katika soko la China au kuagiza mitambo kutoka nchini humo.

Alisema wataalamu kutoka ubalozini watakuwepo muda wote wa maonesho hayo kutoa elimu kuhusu bidhaa zinazohitajika katika soko la China, namna ya kusafirisha bidhaa, kupata vibali pamoja na fursa za uwekezaji na ununuzi wa mitambo ya viwandani.

“Lengo kuu ni kutoa huduma za ushauri kwa Watanzania kuelewa maana halisi ya soko la China, bidhaa gani unaweza kuzipeleka, namna ya kuzipeleka, sheria gani zinahitajika na namna ya kuomba vibali mbalimbali,” alisema.

Aidha, alisema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan imeendelea kusukuma mbele diplomasia ya uchumi kwa lengo la kuongeza uzalishaji, ajira na mapato ya taifa kupitia biashara na uwekezaji.

“China siyo tu soko la bidhaa zetu, bali pia ni chanzo kikubwa cha teknolojia na mitambo inayoweza kusaidia maendeleo ya viwanda vyetu na kuongeza thamani ya bidhaa zinazozalishwa nchini,” alisema.









Paris, Ufaransa
CHUO cha Dhow Countries Music Academy (DCMA) cha Zanzibar kimeandika historia baada ya kutangazwa mshindi wa Tuzo ya 21 ya UNESCO-Sharjah Prize for Arab Culture, katika hafla iliyofanyika Makao Makuu ya UNESCO jijini Paris, Ufaransa. Chuo hicho kimetunukiwa tuzo hiyo kutokana na mchango wake mkubwa katika kuhifadhi, kufundisha na kuendeleza urithi wa muziki wa taarab na tamaduni za ukanda wa Bahari ya Hindi na Kiarabu.

Mwakilishi wa chuo hicho, Bi. Haldah Am Al-Kanaan, alikuwepo Paris kupokea tuzo hiyo kwa niaba ya taasisi. DCMA ni chuo pekee cha muziki Zanzibar kinachojikita katika kufundisha ala za asili na mitindo ya muziki wa jadi ikiwemo taarab, kidumbak na ngoma, huku kikileta pamoja wanafunzi kutoka mataifa mbalimbali na rika tofauti.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mkurugenzi Mkuu wa UNESCO, Profesa Khaled El-Enany, alikipongeza chuo hicho kwa ubunifu wake katika kuhifadhi na kuendeleza urithi wa muziki wa Kiarabu na Kiswahili. Alisema majaji kutoka mabara mbalimbali walivutiwa na namna DCMA ilivyoweza kutumia muziki kama daraja la kuunganisha tamaduni tofauti, pamoja na mazingira yake ya kujifunzia yanayowakutanisha wanafunzi kutoka sehemu mbalimbali duniani.

Kwa upande wake, uongozi wa DCMA ulieleza kuwa tuzo hiyo ni heshima kubwa kwa Zanzibar na Tanzania, na kwamba itakuwa chachu ya kuongeza juhudi katika kulinda na kuendeleza urithi wa taarab na muziki wa jadi kwa vizazi vijavyo.

Hafla hiyo pia ilihudhuriwa na Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Ufaransa na Mwakilishi wa Kudumu katika UNESCO, Balozi Saidi Othman Yakubu, ambaye alishuhudia tukio hilo la kihistoria na kuwapongeza washindi kwa kuitangaza vyema Tanzania kupitia sanaa na utamaduni katika jukwaa la kimataifa.

Tuzo ya UNESCO-Sharjah Prize for Arab Culture, iliyoanzishwa mwaka 1998 kwa ushirikiano kati ya UNESCO na Serikali ya Sharjah, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE), hutolewa kila mwaka kwa watu binafsi au taasisi zilizotoa mchango wa kipekee katika kuendeleza na kutangaza utamaduni wa Kiarabu na kuimarisha mazungumzo ya tamaduni duniani. Katika toleo la mwaka huu, DCMA ilitangazwa mshindi pamoja na mwanamuziki na mjasiriamali wa utamaduni kutoka Morocco, Brahim El Mazned.

Na, Mwandishi Wetu – Dodoma

SERIKALI imesema itaendelea kuimarisha mifumo ya usimamizi wa maafa nchini ili kupunguza madhara yanayosababishwa na majanga mbalimbali ambayo yamekuwa yakigharimu maisha ya watu, kuharibu mali na kurudisha nyuma maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Kauli hiyo imetolewa hii leo 25 Juni, 2026 na Naibu Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Dkt. James Kilabuko, wakati akifunga Jukwaa la Wadau wa Usimamizi wa Maafa lililojadili Rasimu ya Mpango wa Taifa wa Dharura wa Kuzuia na Kukabiliana na Madhara ya El Niño Jijini Dodoma.

Amesema Tanzania imeendelea kukabiliwa na matukio ya maafa yanayosababisha athari kubwa kwa wananchi na uchumi wa Taifa, hali inayolazimu kuwepo kwa maandalizi madhubuti ya kukabiliana na changamoto hizo kabla hazijatokea.

“Nchi yetu imekuwa ikishuhudia matukio ya majanga ambayo yamekuwa yakisababisha maafa na kuathiri mfumo wa kawaida wa maisha ya jamii. Majanga hayo yamesababisha vifo, ulemavu wa kudumu, upotevu wa mali na uharibifu wa miundombinu,” amesema Dkt. Kilabuko.

Amesema kufuatia taarifa ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) ya Aprili 28, 2026 kuhusu uwezekano wa kujitokeza kwa hali ya El Niño, Ofisi ya Waziri Mkuu imeandaa Rasimu ya Mpango wa Taifa wa Dharura kwa ajili ya kuzuia na kukabiliana na madhara yanayoweza kutokea kuanzia Agosti 2026 hadi Juni 2027.

Kwa mujibu wa Dkt. Kilabuko, rasimu hiyo imejadiliwa na wadau mbalimbali ili kuiboresha kwa kuzingatia uzoefu uliopatikana wakati wa matukio ya El Niño yaliyowahi kutokea nchini, hususan ya mwaka 2023/2024.

Amesema ushirikishwaji wa wadau ni hatua muhimu itakayoiwezesha Serikali kuwa na mpango shirikishi na unaotekelezeka katika kuzuia, kujiandaa, kukabiliana na kurejesha hali endapo maafa yatatokea.

“Ni vema kushiriki kikamilifu na kutoa maoni yetu huku tukijielekeza kwenye athari tarajiwa na hatua za kuchukua ili kuwa na mpango thabiti utakaoiwezesha Serikali na wadau kuchukua hatua stahiki za kuzuia au kupunguza madhara,” amesema.

Aidha, ameeleza imani yake kuwa jukwaa hilo litatoa mchango mkubwa katika kuimarisha ufanisi wa usimamizi wa maafa nchini na kuongeza uwezo wa taasisi mbalimbali kukabiliana na changamoto za majanga.

Dkt. Kilabuko amesisitiza kuwa usimamizi wa maafa haupaswi kuonekana kama jukumu la taasisi chache pekee, bali unapaswa kujumuishwa katika mipango ya maendeleo na utekelezaji wa shughuli za kila siku za wizara, taasisi na mamlaka za serikali za mitaa.

Amesema hatua hiyo itasaidia kujenga jamii yenye uwezo wa kuhimili majanga na kulinda maendeleo yaliyopatikana nchini dhidi ya athari zinazoweza kusababishwa na hali ya El Niño na majanga mengine.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu Brigedia Jenerali Hosea Ndagala amesema kuwa,Jukwaa hilo ni muhimu na lipo kisheria hivyo litumike kwa manufaa na kuzingatia umuhimu wake.

Aidha alitumia nafasi hiyo kuzikumbusha kamati za maafa ngazi zote kuendelea kujiandaa na kukabiliana na maafa pindi yanapotokea kwa kuendelea kuweka mipango madhubuti ili kupunguza madhara yanayoweza kujitokeza hasa yale ya uharibifu wa miundombinu na kuepuka madhara mengine kwa jamii na Taifa kwa Ujumla.









Na Belinda Joseph-Dodoma.

Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dkt. Dorothy Gwajima, amezindua rasmi Mwongozo wa Uendeshaji wa Baraza la Taifa la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NaCoNGO) Toleo la Pili, akieleza kuwa hatua hiyo ni muhimu katika kuimarisha utawala bora, uwajibikaji na ufanisi wa sekta ya mashirika yasiyo ya kiserikali nchini Tanzania. 

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Juni 25, 2026, Jijini Dodoma, alisema mwongozo huo utasaidia kuongeza uwazi katika utekelezaji wa majukumu ya viongozi na wanachama wa NaCoNGO, amebainisha kuwa uwepo wa taratibu zilizo wazi utachangia kujenga taasisi imara zinazoweza kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi na kuaminika mbele ya jamii na wadau wa maendeleo.

Ameeleza kuwa lengo kuu la mwongozo huo ni kuainisha taratibu, majukumu, wajibu na mfumo wa uendeshaji wa NaCoNGO ili kuhakikisha utawala bora, uwazi na uwajibikaji katika shughuli zote za Baraza, amesisitiza kuwa taasisi yoyote inayotaka kudumu na kuheshimika lazima ijengwe juu ya misingi ya sheria, maadili na mifumo madhubuti ya utendaji.

Aidha, amesifu muundo wa Baraza unaojumuisha wajumbe 30 wanaowakilisha mikoa yote 26 ya Tanzania Bara pamoja na makundi maalum ya watu wenye ulemavu, watoto, vijana na mashirika ya kimataifa, Kwa mujibu wa Gwajima, muundo huo unaonyesha dhamira ya dhati ya kuhakikisha ushirikishwaji, usawa na uwakilishi mpana wa wadau wote ndani ya sekta ya mashirika yasiyo ya kiserikali.

Katika hotuba yake, Dkt. Gwajima amesisitiza umuhimu wa mgawanyo sahihi wa majukumu kati ya ngazi za Wilaya, Mkoa na Taifa, amesema mwongozo huo umeweka wazi mamlaka ya kila ngazi na namna ya kushirikiana kwa lengo la kuondoa migongano ya kiutendaji, kuongeza ufanisi na kuimarisha uwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu ya Baraza.

Pia ameeleza kuwa toleo hilo la pili limeandaliwa kwa kuzingatia mabadiliko ya kisheria, mazingira ya sasa ya utendaji pamoja na mahitaji mapya ya wanachama na wadau, ameongeza kuwa mwongozo huo ni nyenzo muhimu itakayosaidia kuimarisha uongozi na utendaji wa NaCoNGO katika kipindi hiki cha maendeleo na mageuzi ya taasisi.

Dkt. Gwajima ametoa pongezi kwa viongozi na wanachama wa NaCoNGO kwa kuendelea kushirikiana na Serikali katika kukuza maendeleo ya wananchi, amesema mashirika yasiyo ya kiserikali yana mchango mkubwa katika utoaji wa huduma za kijamii, utetezi wa haki za makundi mbalimbali na kuimarisha ustawi wa jamii, hivyo yanapaswa kuendelea kufanya kazi kwa weledi na uadilifu.

Akihitimisha hotuba yake, Waziri Dorothy Gwajima alitoa wito kwa wajumbe na wadau wote wa sekta kuutumia mwongozo huo kama chombo cha kuimarisha mshikamano, uwajibikaji na ushirikiano, amesema Serikali itaendelea kushirikiana na NaCoNGO katika kujenga sekta imara, yenye kuaminika na yenye mchango mkubwa zaidi katika maendeleo ya Taifa na ustawi wa wananchi kwa ujumla. 







Na Andrea Kadege, WAF-Dar es Salaam


Mkurugenzi wa Shirika la Afya Duniani Ukanda wa Afrika Prof. Mohamed Janabi amesisitiza umuhimu wa ufuatiliaji wa haraka wa wagonjwa na uwekezaji katika mifumo ya afya kama nguzo muhimu ya kudhibiti ugonjwa wa Ebola barani Afrika

Prof. Janabi amesema hayo leo Juni 25, 2026 Jijini Dar es Salaama katika mkutano maalum wa kijadili mustakabali wa kukabiliana na Ugonjwa wa Ebola uliowakutanisha Shirika la Afya Duniani (WHO), Wizara ya Afya na wadau wa maendeleo ambapo Prof. Janabi, alieleza kwa kina mikakati ya kudhibiti ugonjwa wa Ebola, akisisitiza umuhimu wa ufuatiliaji wa haraka wa wagonjwa na uwekezaji thabiti katika mifumo ya afya barani Afrika.

Dkt. Janabi amebainisha kuwa ugonjwa wa Ebola ulitambuliwa kwa mara ya kwanza ncjini DRC, na tangu wakati huo umeendelea kuibua changamoto kubwa za kiafya na kiusalama wa afya ya umma.

Akitaja historia ya milipuko ya awali, amekumbusha mlipuko wa mwaka 2007 katika eneo la Budi Bunya nchini Uganda, ambapo udhibiti wake ulifanikiwa kutokana na uimara wa mfumo wa afya ya umma, na kubainisha kwamba milipuko iliyofuata ilionesha changamoto kubwa zaidi, hasa kutokana na kuchelewa kwa utambuzi wa ugonjwa na mabadiliko ya mwenendo wa maambukizi.

"Moja ya nguzo muhimu katika udhibiti wa Ebola ni ufuatiliaji wa watu waliokutana na wagonjwa (contact tracing), ambapo mafanikio yake hutegemea kiwango cha juu cha ufuatiliaji kinachopaswa kufikia kati ya asilimia 75 hadi 95 na katika baadhi ya maeneo kiwango hicho kimekuwa cha chini, hali inayoongeza hatari ya kuendelea kusambaa kwa maambukizi" amesema Prof. Janabi

Aidha ameeleza kuwa katika baadhi ya matukio, idadi ya watu wanaofuatiliwa inawaweza kuongezeka jambo linaloonyesha ukubwa wa changamoto ya kudhibiti milipuko hiyo akisisitiza umuhimu wa ushirikiano wa karibu kati ya nchi, WHO na wadau wa maendeleo ili kuhakikisha taarifa zinapatikana kwa wakati na hatua za haraka zinachukuliwa.

Kwa upande mwingi amesisitiza kuwa uwekezaji katika sekta ya afya si gharama bali ni uwekezaji wenye manuaa akihimiza kuwa kila hatua ya mapema katika kuzuia milipuko huokoa maisha, hupunguza mzigo wa matibabu na kuimarisha ustahimilivu wa mifumo ya afya barani Afrika.


Na Karama Kenyunko Michuzi Tv


KIJANA,Metson Frank (23) maarufu ‘Mkumbo’ anayeishi Goba Centre wilayani Ubungo amehikumiwa kifungo cha maisha jela baada ya kupatikana na hatia ya kosa la kumlawiti mtoto mwenye umri wa mwaka mmoja na miezi 10.

Hukumu hiyo ya kesi ya jinai namba 28576 ya mwaka 2026 imesomwa Jana ya na Hakimu Mkazi Mwandamizi, Tumsifu Barnabas wa Mahakama Wilaya ya Ubungo.

Kabla ya kusomwa kwa hukumu hiyo, Hakimu Barnabas aliuliza upande wa mashtaka kama walikuwa na lolote la kusema ndipo Wakili wa Serikali Mkuu, Flora Massawe akisaidiana na Wakili wa Serikali Mwandamizi, Agatha Lumato na Wakili wa Serikali, Clemence Mango waliomba mahakama itoe adhabu kali kwa mujibu wa sheria ili iwe fundisho kwa watu wengine wanaofanya ukatili kwa watoto

"Baada ya kusikiliza ushahidi wa pande zote na kufanya uchambuzi wa kina wa ushahidi uliowasilishwa, mahakama unamtia hatiani mshtakiwa kwa kosa la kulawiti kinyume na kifungu cha 154(1)(a)(2) cha Sheria ya Kanuni za Adhabu, Sura ya 16, Marejeo ya mwaka 2023". Alisema Hakimu

Akisoma hukumu huyo Hakimu Barnabas alisema ushahidi wa mashahidi nane na vielelezo vitatu vilivyowasilishwa mahakamani hapo na upande wa mashtaka umeweza kuthibitisha pasipo kuacha shaka kuwa mshtakiwa alitenda kosa hilo.

Amesema, katika hati ya mashataka ilidaiwa Septemba 10, 2025 majira ya usiku mshitakiwa ambaye ni baba wa kufikia wa mtoto huyo, alitenda kitendo hicho akiwa amelala naye katika chumba kimoja.

Hakimu alisema katika maelezo ya onyo ya mshtakiwa yaliyowasilishwa mahakamani hapo yalidai mshtakiwa alikiri kufanya kitendo hicho kwa kuwa mke wake ambaye ni mama wa mtoto aliyefanyiwa ukatili alikuwa ni mjamzito na hivyo alipata hamu ya ghafla.

Iliendelea kuelezwa kuwa mbali na kumlawiti mtoto huyo, mshtakiwa pia alimpiga na kumchapa kwa waya wa umeme ili asipige kelele wala kulia wakati akimfanyia kitendo hicho hali ambayo ilimuachia majeraha mbalimbali yaliyomlazimu kulazwa katika chumba cha wagonjwa mahututi (ICU) kwa muda mrefu.

Aliendelea kueleza kuwa baada ya matibabu, mtoto alipoteza uwezo wa kuona na kuongea.

Akiendelea kuchambua ushahidi wa mashahidi mbalimbali Hakimu Barnabas alieleza kuwa, katika ushahidi wake mama wa mtoto, alidai siku ya tukio walikuwa nyumbani kwa wazazi wa mwanaume eneo la Goba.

Alidai kuwa kutokana na hali yake ya ujauzito, alikwenda kulala huku mume wake akimuomba alale na mtoto huyo katika chumba kingine.

Asubuhi iliyofuata, alibaini kuwa katika chumba alichokuwa amelala mtoto kulikuwa na kinyesi na mtoto alionekana kama anaharisha.

Ilidaiwa kuwa Frank alimweleza hali hiyo mama yake mzazi ambaye walikuwa wanaishi naye, na baada ya kuona mtoto anaendelea kuharisha walimnunulia dawa za kuzuia kuharisha, lakini hali yake iliendelea kuwa mbaya.

Baada ya siku nne, walimpeleka mtoto katika Hospitali ya Taifa Muhimbili akiwa amezimia na kulazwa katika chumba cha wagonjwa mahututi (ICU).

Ilielezwa kuwa uchunguzi wa awali uliofanywa na madaktari ulibaini kuwa mtoto huyo huenda alikuwa amefanyiwa kitendo cha ukatili, kutokana na hali hiyo, madaktari walitoa taarifa katika Kituo cha Polisi Gogoni.

Ilidaiwa askari walifika hospitalini na kuanza uchunguzi mara moja na baada ya uchunguzi Frank alikamatwa nyumbani kwake Goba kwa tuhuma za kumlawiti mtoto huyo.

Hakimu alisema upande wa jamhuri ulihitimisha ushahidi wake na mshitakiwa alikutwa na kesi ya kujibu na katika utete zake alidai kuwa hata yeye alishangaa kuona mtoto ameamka akiwa anaharisha.

Alidai alitoa taarifa kwa watu wa karibu ambao walimshauri mtoto apelekwe hospitali ya Taifa ya Muhimbili na kwamba baada ya siku tatu alishangaa kukamatwa na polisi kuhusiana na tukio hilo.



Top News