Na Seif Mangwangi, Michuzi TV, Arusha,

MAHAKAMA ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu imesema Tanzania imekuwa  ikikiuka baadhi ya haki za msingi za binadamu kwa  kuendelea kutumia adhabu ya kifo ya lazima na utekelezaji wake kwa njia ya kunyongwa.

Hayo yameelezwa Juni5, 2026 Jijini Arusha na majaji wa Mahakama ya Haki za Binaadam na Watu, (AfCPHR), wakiongozwa na Rais wa Mahakama hiyo Jaji Blaise Tchikaya walipokuwa wakisoma hukumu ya kesi nne zilizowasilishwa mahakama hapo  ikiwemo  shauri lililofunguliwa na wafungwa watatu waliohukumiwa kifo kwa kosa la mauaji.

Aidha Mahakama hiyo imewamuru waombaji watatu katika shauri hilo kulipwa fidia ya Shilingi 300,000 kila mmoja kwa madhara ya kimaadili yaliyotokana na ukiukwaji wa haki zao.

 Uamuzi huo umeonyesha Serikali ya Tanzania ilishindwa kutekeleza wajibu wake wa kulinda na kuheshimu haki za binadamu katika eneo la utoaji na utekelezaji wa adhabu ya kifo kwa mujibu wa viwango vya kimataifa vya haki za binadamu.

Hukumu hiyo ilitolewa mjini Arusha katika kesi iliyowahusisha Godfrey Gabinus Ndimba na wenzake wawili dhidi ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambapo waombaji hao walikuwa wamefungwa katika Gereza la Wilaya ya Lindi wakisubiri utekelezaji wa adhabu ya kifo baada ya kutiwa hatiani kwa kosa la mauaji.

Katika maombi yao, waombaji hao walidai kuwa haki zao zilikiukwa wakati wa uchunguzi, usikilizwaji na utoaji wa hukumu katika mahakama za ndani. Walieleza kuwa kulikuwa na kasoro mbalimbali zilizowaathiri katika kupata haki stahiki.

Mahakama hiyo ya Afrika ilibaini kuwa Serikali ya Tanzania haikuwasilisha majibu yoyote katika shauri hilo licha ya kupewa taarifa zote muhimu na muda wa kutosha kufanya hivyo na  kutokana na hali hiyo, Mahakama iliamua kutoa hukumu kwa kutokuwepo kwa upande wa Serikali.

Kabla ya kuamua shauri hilo, Mahakama ilijiridhisha kuwa ilikuwa na mamlaka ya kusikiliza kesi hiyo na kubaini kuwa madai yaliyowasilishwa yalihusu haki zinazolindwa chini ya Mkataba wa Afrika wa Haki za Binadamu na Watu pamoja na mikataba mingine ya kimataifa iliyoridhiwa na Tanzania.

Mahakama pia ilikubaliana kuwa waombaji walikuwa wametumia njia zote za ndani za kutafuta haki, ikiwemo kukata rufaa katika Mahakama ya Rufani ya Tanzania kabla ya kufikisha shauri lao katika Mahakama ya Afrika.

Katika uchambuzi wa madai ya ukiukwaji wa haki ya kusikilizwa kwa haki, Mahakama ilibaini kuwa waombaji hawakuwasilisha ushahidi wa kutosha kuthibitisha madai yao kuhusu kutengenezwa kwa ushahidi, uwakilishi wa kisheria na mwenendo wa kesi zao. Kutokana na hali hiyo, madai hayo yalitupiliwa mbali.

Kadhalika, madai ya ukiukwaji wa haki ya usawa mbele ya sheria yalikataliwa baada ya Mahakama kubaini kuwa hayakuungwa mkono na ushahidi wa kutosha kuthibitisha kuwa waombaji walitendewa tofauti au kunyimwa ulinzi sawa wa kisheria.

Hata hivyo, Mahakama ilikubaliana na hoja kwamba utoaji wa adhabu ya kifo kwa lazima bila kuzingatia mazingira ya kila mshtakiwa ni ukiukwaji wa haki ya kuishi inayolindwa chini ya Kifungu cha 4 cha Mkataba wa Afrika wa Haki za Binadamu na Watu.

Mahakama pia ilieleza kuwa utekelezaji wa adhabu ya kifo kwa njia ya kunyongwa ni ukiukwaji wa haki ya utu wa binadamu na heshima ya mtu kama ilivyoainishwa katika Kifungu cha 5 cha Mkataba huo.

Kutokana na maamuzi hayo, Mahakama ilihitimisha kuwa Tanzania ilikiuka wajibu wake chini ya Kifungu cha 1 cha Mkataba wa Afrika wa Haki za Binadamu na Watu. Hata hivyo, Mahakama ilikataa maombi ya kufutwa kwa hukumu za ndani na kuwaachia huru waombaji, huku ikisisitiza kuwa fidia ya Shilingi 300,000 kwa kila mmoja ilikuwa hatua stahiki ya kurekebisha madhara ya ukiukwaji wa haki zilizobainika.





Na Mwandishi Wetu

MKURUGENZI Mkuu wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), Dkt. Immaculate Sware Semesi, amesema uhifadhi wa mazingira ni jukumu la kila mwananchi kwa kuwa athari za uharibifu wa mazingira huathiri moja kwa moja maisha ya binadamu na maendeleo ya taifa.

Dkt. Semesi ametoa kauli hiyo wakati akizungumza na wanafunzi katika kilele cha maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani yaliyofanyika jijini Dodoma.

Amesema NEMC inaendelea kutekeleza mikakati mbalimbali inayolenga kubadili mtazamo wa wananchi kuhusu taka kwa kuzifanya kuwa fursa za kiuchumi kupitia ukusanyaji, uchakataji na uzalishaji wa bidhaa mbalimbali zinazotokana na taka.

Kwa mujibu wa Dkt. Semesi, hatua hiyo inalenga kusaidia kulinda mazingira huku ikiongeza kipato kwa wananchi kupitia shughuli za urejelezaji na uchumi wa mzunguko.

Aidha, amesema NEMC imejipanga kuendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa kulinda na kuhifadhi mazingira ili yaendelee kutoa huduma muhimu za kiikolojia, fursa za kiuchumi na kuchangia maendeleo endelevu ya nchi.

Aliongeza kuwa maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani yamekuwa jukwaa muhimu la kuelimisha umma kuhusu masuala ya mazingira pamoja na kutoa ushauri wa kitaalamu unaolenga kuboresha huduma za usimamizi na uhifadhi wa mazingira nchini.

Dkt. Semesi amewahimiza wanafunzi na wananchi kwa ujumla kushiriki kikamilifu katika shughuli za utunzaji wa mazingira, ikiwemo upandaji miti, usimamizi bora wa taka na matumizi endelevu ya rasilimali za asili ili kuhakikisha mazingira salama kwa kizazi cha sasa na kijacho.

Mkurugenzi Mkuu wa NEC Immaculate Semes akiwa Katika picha ya pamoja kilele cha maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani.
-Wananchi wa zaidi 400 wapata elimu ya uhifadhi wa mazingira kutoka NEMC Dodoma.

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Zaidi ya wananchi na wadau 400 wametembelea banda la Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) na kupata elimu kuhusu uhifadhi wa mazingira katika maadhimisho ya Wiki ya Mazingira Duniani yaliyofanyika jijini Dodoma.

Meneja wa Kanda ya Kati wa NEMC, Novatus Mushi, amesema mwitikio huo unaonesha kuongezeka kwa uelewa wa wananchi kuhusu umuhimu wa kuhifadhi mazingira na mchango wa elimu katika kubadili mitazamo ya jamii kuelekea maendeleo endelevu.

Akizungumza katika kilele cha maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani yaliyofanyika katika Ukumbi wa Jakaya Kikwete Convention Centre (JKCC) Juni 5, 2026, Mushi alisema NEMC imeendelea kutumia mifumo ya kisasa ya kidijitali katika kusimamia na kufuatilia mazingira kwa wakati halisi.

Alisema miongoni mwa mifumo hiyo ni teknolojia inayowezesha kutambua viashiria vya uchafuzi wa mazingira mara vinapotokea, hatua inayorahisisha ufuatiliaji na kuchukua hatua stahiki kwa wakati.

“Tunazo mifumo ya kisasa ya usimamizi wa mazingira ya kidijitali. Mfumo huu mpya unatuwezesha kuona dalili za uchafuzi wa mazingira kwa wakati halisi na hivyo kuongeza ufanisi katika usimamizi wa mazingira,” alisema Mushi.

Aidha, alisema NEMC inaendelea kutumia Mfumo wa Usimamizi wa Miradi (PMS) unaorahisisha utoaji wa vibali vya Tathmini ya Athari kwa Mazingira (EIA) kwa miradi mbalimbali ya maendeleo kabla ya kuanza kutekelezwa.

Kwa mujibu wa Mushi, matumizi ya mifumo hiyo yamechangia kuongeza uwazi, kupunguza muda wa utoaji huduma na kuimarisha usimamizi wa mazingira nchini.

Amesema maonyesho hayo yamewapa fursa wadau na wananchi kujifunza namna teknolojia inavyoweza kutumika katika kulinda mazingira na kuhimiza maendeleo yanayozingatia uhifadhi wa rasilimali za asili.

Mushi pia alisema NEMC inaendelea kushirikiana na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) katika kubadilishana taarifa na takwimu za hali ya hewa na mazingira ili kusaidia kupanga na kutekeleza miradi kwa kuzingatia athari za mabadiliko ya tabianchi.

Alieleza kuwa ushirikiano huo unasaidia kufanya maamuzi sahihi ya maendeleo na kuzuia hasara kubwa za kiuchumi ambazo zinaweza kujitokeza endapo miradi itatekelezwa bila kuzingatia taarifa muhimu za hali ya hewa na mazingira.

Akizungumzia mwelekeo wa NEMC kuwa mamlaka kamili, alisema hatua hiyo itasaidia kuimarisha ufanisi wa utendaji kazi, kupunguza urasimu na kuongeza kasi ya utekelezaji wa majukumu ya usimamizi wa mazingira.

“Mazingira, watu na uchumi lazima viendane. Tukipata mamlaka kamili tutaongeza ufanisi wa utendaji kazi na kuboresha huduma kwa wananchi,” alisema.

Hata hivyo, alisema Kanda ya Kati inayojumuisha mikoa ya Dodoma, Singida na Iringa bado inakabiliwa na changamoto mbalimbali za mazingira, ikiwemo migogoro ya matumizi ya ardhi, matumizi ya teknolojia duni katika shughuli za kiuchumi na uelewa mdogo wa baadhi ya wananchi kuhusu umuhimu wa uhifadhi wa mazingira.

Alisema NEMC itaendelea kuimarisha utoaji wa elimu kwa umma, usimamizi wa sheria za mazingira na ufuatiliaji wa shughuli mbalimbali ili kuhakikisha rasilimali za mazingira zinahifadhiwa kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Mkurugenzi Mkuu wa NEC Immaculate Semes akiwa  Katika picha ya wanafunzi akifanya mazungumzo wanafunzi waliokuwa wakitoa elimu ya uhifadhi wa mazingira katika    kilele cha maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani mjini Dodoma



Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Mussa Azan Zungu ametembelea na kukagua maendeleo ya ujenzi wa Shule ya Sekondari ya Mfano ya Benki ya CRDB (CRDB Bank Secondary Model School) inayojengwa Upanga katika Halmashauri ya Ilala.

Mheshimiwa Zungu aliyepokelewa na Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Benki ya CRDB na Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB Bank Foundation, TullyEsther Mwambapa amepongeza kasi ya mkandarasi na kumuomba akamilishe ujenzi mapema iwezekanavyo ili kuwanufaisha wanafunzi wanaotarajiwa kujiunga.

"Shule hii inajengwa Ilala ila itawahudumia wanafunzi kutoka kila mahali. Nampongeza Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Dkt. Abdulmajid Nsekela na menejimenti nzima kwa kuona umuhimu wa kujenga shule hii itakayowafaa watoto wa Kitanzania. Nikuombe mkandarasi, ongeza kasi ujenzi ukamilike mapema," amesema Spika Zungu.

Akieleza maendeleo ya mradi huo, Tully amesema utakagharimu jumla ya shilingi bilioni 5. "Itakuwa shule bora na ya kisasa. Tunashukuru serikali ya Manispaa ya Ilala kwa kutuamini na kushirikiana nasi kuboresha maisha ya wananchi," amesema Tully.

Kuhusu kukamilika kwa ujenzi huo, Mhandisi Anna Mafoka, mkandarasi anayeujenga mradi huo amesema mkataba ulitaka shule hoyo ijengwe kwa miezi 10 na kukamilika Machi mwakani lakini watajitahidi majengo yawe tayari kwa matumizi ifikapo Desemba ili Januari yaanze kutumika.












Farida Mangube, Morogoro

Wataalamu wameonya kuwa kuongezeka kwa matumizi ya kemikali za kilimo bila kuzingatia kanuni za kitaalamu kunaweza kuongeza hatari ya magonjwa, kuathiri ubora wa mazao na kuhatarisha mazingira, wakitaka wakulima kuelekea zaidi katika matumizi ya mbinu za kilimo ikolojia.

Akizungumza katika mkutano ulioandaliwa na Sekretarieti ya Kitovu cha Kilimo Ikolojia kupitia Mradi wa Mtandao wa Utafiti wa Ikolojia Kusini mwa Afrika (RAENS) mkoani Morogoro, Profesa Kalunde Sibuga wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) alisema matumizi yasiyo sahihi ya kemikali yanaweza kuathiri afya za wakulima, walaji na mazingira, huku mabaki ya kemikali kwenye mazao yakihatarisha usalama wa chakula.

Alisema kilimo ikolojia ni suluhisho linaloweza kuongeza uzalishaji wa mazao kwa kutumia mbinu rafiki kwa mazingira kama mbolea za asili, udhibiti wa wadudu kwa njia za kibaiolojia na usimamizi endelevu wa ardhi na maji, akisisitiza umuhimu wa kutoa elimu kwa wakulima kuhusu matumizi salama ya pembejeo.

Kwa upande wake, Mratibu wa RAENS, Profesa Dismas Mwaseba, alisema pamoja na uwepo wa sera zinazounga mkono kilimo endelevu, bado sekta hiyo inakabiliwa na changamoto zikiwemo ukosefu wa masoko ya uhakika, uelewa mdogo wa wakulima na upungufu wa huduma za mafunzo na ugani kuhusu kilimo ikolojia.

Naye mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Bw. Gosbert Chobya, alisema Serikali inaendelea kutambua mchango wa kilimo ikolojia katika kuongeza tija, kulinda mazingira na kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, huku akisisitiza ushirikiano wa wadau mbalimbali katika kuboresha sera na mazingira ya utekelezaji wa kilimo hicho nchini.






Na ABDU MADENGE, WAF - DODOMA

Baraza la Tiba Asili na Tiba Mbadala nchini limefuta usajili wa dawa ya Powaful Banana Medicine, kupiga marufuku uingizwaji na matumizi ya dawa ya Vitamax, pamoja na kuamuru kuondolewa sokoni kwa toleo namba MN1060 la dawa ya Joy.

Hatua hiyo imechukuliwa baada ya ukaguzi na vipimo vya maabara kubaini uwepo wa mchanganyiko wa kemikali hatari za kisasa na sumu kuvu kwenye bidhaa hizo kinyume cha sheria.

Hayo yamebainishwa na Mwenyekiti wa Baraza hilo, Prof. Nicolao Joseph Otieno, wakati wa mkutano na waandishi wa habari uliofanyika katika Ofisi za Wizara ya Afya Juni 05, 2026 Mkoani Dodoma ambapo ameeleza maamuzi hayo yanajiri kufuatia zoezi maalum la ufuatiliaji wa dawa sokoni (Post Market Surveillance) lililofanyika katika mwaka wa fedha wa 2025/2026, ambalo lilibaini ukiukwaji mkubwa wa Kanuni za Usimamizi wa Dawa za Tiba Asili kifungu cha 13(1)(a) na (b).

Prof. Otieno ameongeza kuwa Uchunguzi wa kimaabara umeonesha dawa ya Powaful Banana (inayotengenezwa na Powaful Products Company Ltd) na Vitamax (kutoka kampuni ya Superfood International ya Malaysia), ambazo zimekuwa zikitumika kuongeza nguvu za kiume, zimechakachuliwa kwa kuongezewa kemikali za kisasa za Sildenafil, Tadalafil, pamoja na dawa za maumivu aina ya Tramadol na Paracetamol.

“Tunaonya matumizi ya kemikali hizo bila usimamizi wa daktari yanaweza kusababisha magonjwa ya moyo, kufeli kwa ini na figo, shinikizo la damu, na hata vifo vya ghafla.” amesema Prof . Otieno.

Sambamba na hatua hizo, Baraza pia limebaini kuwa toleo namba MN1060 la dawa ya Joy (Usajili Na. TZ25TM0010) lina kiwango kikubwa cha sumu kuvu (mycotoxins) kinachoweza kusababisha saratani ya ini na uharibifu wa figo. Hali hii imetajwa kutokana na kutokuzingatiwa kwa viwango bora vya ukaushaji na uhifadhi wakati wa uzalishaji.

“Baraza tunatoa onyo kali kwa watengenezaji wote nchini ambao dawa zao zimebainika kuwa na mapungufu katika vifungashio, taarifa za lebo, ujazo, na maelezo ya dozi, tunawataka kufanya maboresho ya haraka kulingana na vigezo vya usajili kwa lengo la kulinda afya na usalama wa watumiaji.” amesema na kuongeza Prof. Otieno.





 

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, , amewataka wanafunzi wa sheria nchini kujenga taaluma zao katika misingi ya nidhamu, ubunifu na uzalendo ili waweze kushindana katika soko la ajira la kimataifa linalozidi kuwa na ushindani.

Ridhiwani alitoa wito huo Juni 5, 2026, alipokuwa akizungumza katika maadhimisho ya Siku ya Kazi na Taaluma ya Shule ya Sheria ya yaliyofanyika jijini Dar es Salaam.

Alisema mafanikio katika taaluma za kisasa hayawezi kupatikana bila wataalamu kuzingatia maadili, hususan nidhamu, uzalendo na umahiri wa kitaaluma, mambo ambayo ni muhimu katika kujenga uwezo wa kushindana ndani na nje ya mipaka ya nchi.

“Ni muhimu kwa wanafunzi wa sheria kutambua kuwa dunia ya sasa inahitaji wataalamu wenye uwezo wa kushindana kimataifa huku wakizingatia maadili ya taaluma zao na kulinda maslahi ya taifa lao,” alisema.

Aidha, Ridhiwani alisema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia imeendelea kufanya mageuzi makubwa katika sekta ya sheria na haki kwa lengo la kuimarisha utoaji wa huduma za haki nchini.

Alitaja baadhi ya hatua zilizochukuliwa kuwa ni pamoja na matumizi ya teknolojia katika mfumo wa haki, uwekezaji katika miundombinu ya utoaji haki pamoja na kuhamasisha matumizi ya mifumo mbadala ya utatuzi wa migogoro.

Kwa mujibu wa Ridhiwani, mageuzi hayo yanalenga kuwawezesha wanasheria na watendaji wa vyombo vya haki jinai kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi huku yakichangia kujenga mazingira bora ya maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

Alisisitiza kuwa wataalamu wa sheria wana nafasi muhimu katika kulinda maslahi ya taifa, kuimarisha utawala wa sheria na kuchochea maendeleo endelevu kupitia usimamizi wa haki na sheria.

Maadhimisho hayo yalikusanya wanafunzi, wahadhiri na wadau mbalimbali wa sekta ya sheria kujadili fursa na changamoto zinazokabili taaluma hiyo katika mazingira ya dunia yanayobadilika kwa kasi.
Na Beda Msimbe, TBN, aliyekuwa Urusi

IJUMAA, Juni 5, 2026, ilikuwa siku ya kihistoria na ya kipekee wakati Rais wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, alipokuwa akizungumza mbele ya viongozi wa dunia katika Jukwaa la Kimataifa la Uchumi la St. Petersburg (St. Petersburg International Economic Forum) na kuwasilisha hoja nzito zenye mashiko, akibeba sauti ya Watanzania wote huku akiweka wazi fursa zinazopatikana Tanzania pamoja na mwelekeo mpya wa nchi katika kujenga uchumi wa kisasa.

Jukwaa hilo lilikuwa sehemu muhimu ya ziara ya Rais Samia ambayo haikuwa tu ya kiitifaki, bali pia ya kufungua milango ya fursa za kiuchumi na kijamii.

Jinsi Rais Samia alivyopokewa na kukirimiwa nchini Urusi katika shughuli zote zilizomhusu, ilionesha taswira ya urafiki wa dhati na uelewano mkubwa kati yake na mwenyeji wake, Rais Vladimir Putin. Ziara hiyo ilifufua historia ya ushirikiano wa mataifa hayo mawili na kuweka wazi haja ya sasa ya kusaidiana katika kuleta ukombozi wa kiuchumi na ustawi wa jamii baada ya ukombozi wa kisiasa.

Akiwa katika jukwaa hilo la kiuchumi, hotuba ya Rais Samia iliwafanya washiriki wengi kutafakari kwa kina kutokana na hoja zake zilizojikita katika uchambuzi wa masuala ya dunia na umuhimu wa mabadiliko ya kimfumo katika uchumi wa kimataifa.

Rais Samia alitoa hoja yenye kuchokoza fikra aliposema kuwa ifikapo mwaka 2050, mtu mmoja kati ya wanne duniani atakuwa Mwafrika. Takwimu hiyo iliambatana na swali lenye uzito mkubwa: “Je, Afrika itastawi na kukua kwa masharti ya nani, na kwa modeli ipi ya uchumi?”

Swali hilo lilikuwa na mantiki kubwa katika kipindi ambacho siasa za kijiografia zimeendelea kuyumbisha ushirikiano wa kawaida wa kimataifa na kujaza mazingira ya masharti, ushindani na udhibiti wa kiuchumi unaozikandamiza nchi maskini.

Katika msingi huo wa kimantiki, Rais Samia alikuwa akiitaka dunia isiisitiri Afrika wala kuipangia mustakabali wake, bali itambue ukweli na kuiacha Afrika ijiamulie mambo yake yenyewe.

Mathalani, Afrika kwa sasa ina Ajenda 2063 pamoja na soko la pamoja la AfCFTA, lakini bado kuna mataifa yanayoendelea kuingilia masuala ya bara hilo na kuwagawa Waafrika ili waendelee kuonekana wanahitaji msaada wa kudumu katika kutatua changamoto zinazowakabili.

Rais Vladimir Putin aliunga mkono hoja hiyo, jambo lililoibua miguno ya ridhaa na vigelegele ukumbini. Kwa hakika, yapo mambo mengi ambayo Waafrika wanaweza kuyafanya wenyewe kwa manufaa yao na ya dunia kwa ujumla.

Mambo yaliyoguswa

Katika hotuba yake na ziara hiyo ya Urusi, Rais Samia aligusa masuala mengi muhimu. Hapa tunaweza kuangazia maeneo makubwa yaliyobebwa na ziara hiyo pamoja na namna makubaliano mbalimbali yalivyohitimishwa kwa mafanikio makubwa kwa Tanzania.

Ikumbukwe kuwa ziara ya Rais Samia, ambayo pia aliambatana na wafanyabiashara wa Tanzania, imeikumbusha dunia kuhusu mizizi imara ya kidiplomasia kati ya Tanzania na Urusi. Mahusiano hayo yana historia ndefu tangu miaka ya mwanzo ya uhuru, ambapo siku mbili tu baada ya Tanganyika kupata uhuru, Urusi ilituma salamu za pongezi; hali iliyojirudia pia wakati wa Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar.

Mbele ya wawekezaji, Rais Samia alibainisha kuwa uchumi wa Tanzania unakua kwa kasi ya takribani asilimia sita, hali inayoiweka nchi miongoni mwa uchumi unaokua kwa kasi zaidi barani Afrika.

Aidha, alitangaza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayolenga kumfikisha kila Mtanzania kwenye kipato cha wastani cha dola za Marekani 7,000 huku akielezea kwa kina fursa mbalimbali za uwekezaji na biashara zilizopo nchini Tanzania.

Hotuba hiyo iliyopigiwa makofi mara kwa mara iliwavutia wawekezaji wengi wa Kirusi, ambapo sekta binafsi ya Urusi ilikiri kuwa Tanzania ni soko salama lenye utulivu wa kisiasa unaowezesha ukuaji wa mitaji na biashara.

Mbali na hayo, Rais Samia alieleza kuhusu mapinduzi makubwa ya miundombinu yanayoendelea nchini, hususan katika sekta ya reli na bandari. Katika mikutano ya pamoja na wafanyabiashara wa Tanzania na Urusi, alifafanua kwa kina kuhusu ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR) inayounganisha Bandari ya Dar es Salaam na nchi za Rwanda, Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), pamoja na manufaa yake kwa ukanda mzima wa Afrika Mashariki na Kati.

Pia alieleza mpango wa miaka mitano wa kuipanua reli hiyo kuanzia mwaka 2026 hadi 2031 kuelekea Musoma na kuunganisha ukanda wa kusini kupitia Malawi hadi Msumbiji. Urusi, ikiwa na uzoefu mkubwa katika teknolojia ya reli na usafirishaji, ilionesha nia ya kutoa utaalamu wa kihandisi pamoja na mitambo ya kusaidia kuharakisha ujenzi wa reli hizo za kikanda.

Suala la maboresho ya mazingira ya uwekezaji na mfumo wa usajili wa saa 24 lilizua msisimko mkubwa miongoni mwa washiriki. Rais Samia alieleza kuwa uwekezaji umeongezeka kutoka dola bilioni tatu mwaka 2021 hadi dola bilioni 12 mwaka 2025 kutokana na maboresho ya mifumo ya uwekezaji, ikiwemo usajili wa kampuni unaokamilika ndani ya saa 24.

Kutokana na mafanikio hayo, Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) pamoja na taasisi za uwekezaji za Urusi zilisaini mikataba ya ushirikiano. Hatua hiyo ilipokelewa kwa furaha kubwa, ikionesha namna Tanzania ilivyojidhatiti kupunguza urasimu katika uwekezaji.

Aidha, miradi ya Eneo Maalum la Kiuchumi la Bagamoyo pamoja na Bandari ya Kimataifa ya Mizigo ya Mangapwani Zanzibar ilipewa kipaumbele na makampuni makubwa ya Urusi yanayojihusisha na usafirishaji wa baharini. Makampuni hayo yalikubali kutuma timu za wataalamu nchini Tanzania kufanya upembuzi yakinifu wa namna ya kuwekeza katika miradi hiyo.

Katika sekta ya madini, Rais Samia alisisitiza umuhimu wa kuongeza thamani ya madini ndani ya nchi. Tanzania ina utajiri mkubwa wa dhahabu, uranium, nickel, graphite, helium pamoja na madini adimu.

“Hatutaki tena kuuza malighafi pekee; tunataka viwanda vya usindikaji hapa nchini,” alisema Rais Samia.

Urusi, ambayo ni miongoni mwa mataifa yenye nguvu katika sekta ya madini, ilionesha utayari wa kushirikiana na Tanzania katika kujenga viwanda vya uchakataji na kuongeza thamani ya madini kabla ya kusafirishwa kwenda nje ya nchi.

Katika ziara hiyo, Rais Samia alidhihirisha wazi namna Tanzania ilivyo tayari kwa biashara, ubunifu na ushirikiano wa kimataifa unaolenga kukuza uchumi na ustawi wa wananchi wake.

Wakati Rais Samia akihitimisha hotuba yake katika jukwaa la St. Petersburg kwa kutoa shukrani za dhati kwa Rais Vladimir Putin kwa ukarimu wake, viongozi hao wawili walionesha tabasamu la furaha, ishara iliyotafsiriwa kama mwanzo mpya wa ushirikiano wa dhahabu kati ya Tanzania na Urusi.

Na Mwandishi Wetu

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Ridhiwani Kikwete, amewataka wanafunzi wa sheria nchini kujenga taaluma zao katika misingi ya nidhamu, ubunifu na uzalendo ili waweze kushindana katika soko la ajira la kimataifa linalozidi kuwa na ushindani mkubwa.

Ridhiwani alitoa wito, wakati akizungumza katika hafla ya Siku ya Kazi na Taaluma ya Shule ya Sheria ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam iliyofanyika jijini Dar es Salaam.

Alisema mafanikio ya taaluma katika dunia ya sasa hayawezi kupatikana bila wataalamu kuwa na uwezo wa kushindana nje ya mipaka ya nchi zao huku wakizingatia maadili ya kazi, hususan nidhamu, uzalendo na umahiri katika fani zao.

“Ni muhimu kwa wanafunzi wa sheria kuelewa kuwa taaluma zao zinahitaji siyo tu maarifa ya kisheria, bali pia maadili, nidhamu na uzalendo vitakavyowasaidia kuwa wataalamu wenye ushindani na mchango chanya kwa taifa,” alisema.

Aidha, Ridhiwani aliwaeleza wanafunzi hao kuhusu hatua zilizochukuliwa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Samia Suluhu Hassan katika kuimarisha sekta ya sheria na utoaji wa haki nchini.

Alisema serikali imeendelea kufanya mageuzi mbalimbali ikiwemo kuboresha mfumo wa haki, kuongeza matumizi ya teknolojia katika utoaji wa huduma za kisheria, kuwekeza katika miundombinu ya utoaji haki na kuhamasisha matumizi ya mifumo mbadala ya utatuzi wa migogoro.

Kwa mujibu wa Ridhiwani, maboresho hayo yanalenga kuwawezesha wanasheria na wasimamizi wa vyombo vya haki jinai kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi, sambamba na kujenga mazingira bora ya utoaji haki nchini.

Alisisitiza kuwa sekta imara ya sheria na haki ni nguzo muhimu katika kuharakisha maendeleo ya kiuchumi na kijamii, huku wataalamu wa sheria wakibeba jukumu kubwa la kulinda maslahi ya taifa na kuimarisha utawala bora.






BODI ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA) imeshiriki katika Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Jukwaa la Wasimamizi wa Taaluma ya Ukaguzi Afrika (African Forum of Independent Accounting and Auditing Regulators (AFIAAR) wa mwaka 2026, unaofanyika mjini Port Louis, Mauritius kuanzia tarehe 2 hadi 5 Juni 2026.

Katika Mkutano huo, Mkurugenzi Mtendaji wa NBAA, CPA Prof. Siasa Mzenzi, alichaguliwa kuwa Makamu Mwenyekiti wa AFIAAR. Pamoja na Mkurugenzi Mtendaji, NBAA imewakilishwa na CPA Pius Maneno, Mkurugenzi Mtendaji Mstaafu wa NBAA na Makamu Mwenyekiti anayemaliza muda wake wa jukwaa hilo; CPA Winnington Makaka, Mkuu wa Sehemu ya Ubora wa Ukaguzi (AQR); pamoja na Magreth Kageya, Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na Mawasiliano cha NBAA.

Lengo la mkutano huo ni kuwakutanisha wasimamizi wa taaluma ya Uhasibu na Ukaguzi barani Afrika ili kujadili masuala mbalimbali yanayohusu taaluma hiyo, hususan hali ya ubora wa ukaguzi. Majadiliano hayo yanalenga kuimarisha ubora wa taarifa za ukaguzi wa makampuni, jambo litakalosaidia kukuza uchumi wa Afrika kwa kuongeza imani ya wawekezaji kupitia taarifa sahihi na za kuaminika za kifedha.

Akizungumza katika mkutano huo, Mkurugenzi Mtendaji wa NBAA na Makamu Mwenyekiti wa AFIAAR, CPA Prof. Siasa Mzenzi, alisema: “Mkutano huu ni muhimu kwa taasisi yetu na Tanzania kwa ujumla, kwani umetupatia fursa ya kujifunza na kubadilishana uzoefu kuhusu mbinu bora za usimamizi wa taaluma ya ukaguzi. Maarifa haya yatasaidia kuboresha ubora wa huduma za ukaguzi nchini na hivyo kuongeza uaminifu wa taarifa za kifedha zinazotolewa na taasisi na makampuni mbalimbali.”

Mkutano wa AFIAAR unawakutanisha wadau mbalimbali wa usimamizi wa taaluma ya ukaguzi kutoka nchi mbalimbali za Afrika kwa lengo la kuimarisha ushirikiano, kubadilishana uzoefu na kujadili mikakati ya kuendeleza ubora wa ukaguzi barani humo.











Pamela Mollel, Arusha

Kampuni ya House of Canvas Ltd imewataka wadau mbalimbali kujitokeza kwa wingi kutembelea banda lake katika Maonesho ya Karibu-Kilifair 2026 na kujionea bidhaa zake zenye ubora wa hali ya juu, uimara na uwezo wa kudumu kwa muda mrefu

Akizungumza na waandishi wa habari katika maonesho hayo yanayoendelea mkoani Arusha, Mkurugenzi wa kampuni hiyo, Evans Ogiloh, amesema kuwa mwaka huu wamekuja na bidhaa mpya nyingi za kisasa zilizoboreshwa ili kukidhi mahitaji ya wateja wa ndani na nje ya nchi

Amesema House of Canvas Ltd imejijengea sifa ya kuzalisha bidhaa bora na zinazodumu kwa muda mrefu, jambo ambalo limeifanya kampuni hiyo kuendelea kuaminika na wateja wake katika sekta mbalimbali

"Mwaka huu tumekuja na bidhaa mpya nyingi zenye ubora wa hali ya juu na zinazodumu kwa muda mrefu

Tunawaalika wadau wote kutembelea banda letu ili wajionee ubunifu na ubora wa bidhaa tunazozalisha," amesema Ogiloh

Aidha, amewapongeza waandaaji wa Maonesho ya Karibu-Kilifair 2026 kwa maandalizi mazuri yaliyofanyika mwaka huu, akibainisha kuwa yameboreshwa kwa kiwango kikubwa ikilinganishwa na mwaka uliopita

"Kwa kweli nimefurahishwa sana na maandalizi ya maonesho ya mwaka huu. Waandaaji wamejipanga vizuri na mazingira ya maonesho ni bora zaidi kuliko mwaka jana," ameongeza

Ogiloh amesema kampuni hiyo inajishughulisha na utengenezaji wa mahema mbalimbali ikiwemo mahema ya kambi za milimani, mahema ya utalii pamoja na bidhaa nyingine za canvas zinazotumika katika shughuli mbalimbali.

Amesisitiza kuwa House of Canvas Ltd itaendelea kubuni na kuzalisha bidhaa zenye viwango vya juu vya ubora ili kukidhi mahitaji ya soko na kuchangia maendeleo ya sekta ya utalii na biashara nchini.






Mkurugenzi wa Kadama English Medium Primary School, Leticia Pastory, ameibuka mshindi wa Tuzo ya Mmiliki Bora wa Shule wa Kike Mkoa wa Geita kwa mwaka 2026. Tuzo hiyo imetolewa kwa kutambua mchango wake mkubwa kwenye sekta ya elimu.

Tuzo ilikabidhiwa rasmi Juni 6, 2026 na Mwenyekiti wa UWT Taifa na Mbunge, Mary Chatanda, kwenye Tamasha la Mwanamke wa Dhahabu 2026 lililofanyika Golden Social Hall, Geita. Tukio hilo liliandaliwa na Geita Women and Youth Foundation inayoongozwa na Mkurugenzi Cecylia Miraji.

Hafla hiyo muhimu ilihudhuriwa na Mkuu wa Mkoa Martine Shigela, Mbunge wa Geita Mjini Chacha Wambura, na Mkurugenzi wa Manispaa Yefred Myenzi.

Baada ya kupokea tuzo, Leticia alisema mafanikio hayo yanatokana na jitihada za miaka mingi za kuinua elimu Geita. Alibainisha kuwa Kadama imejijengea heshima kitaifa kutokana na matokeo mazuri na mazingira bora ya masomo.

Alikumbusha kuwa mwaka 2018 shule hiyo iliweka historia baada ya mwanafunzi wake kushika nafasi ya kwanza kitaifa na mwingine wa pili kwenye matokeo ya darasa la saba.

"Ni faraja kubwa. Tuzo hii inatupa nguvu kuendelea kutoa elimu bora na kuhamasisha wanawake wenzangu watumie nafasi zao kuleta mabadiliko," alisema Leticia.










Top News