Kampuni ya Sandaland Fashion Wear Limited  imetangaza kuchukua hatua za kisheria dhidi ya kauli iliyotolewa hadharani na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda, kuhusu jezi za Timu ya Taifa ya Tanzania, Taifa Stars.

Hatua hiyo imetangazwa kupitia tamko rasmi la kampuni hiyo, baada ya kauli ya Makonda iliyotolewa Septemba 16, 2026 kupitia akaunti yake ya Instagram, ambapo alidai kuwa imeathiri jina, chapa, hadhi na uhalali wa bidhaa za Sandaland katika soko.

Katika ujumbe huo, Makonda alinukuliwa akisema:

“Hii sio jezi ya Taifa Stars, Taifa Stars kwa ubora wake hatuwezi kuwa na jezi za kiwango chini hivi. Acheni kutumia picha za Naibu wangu huku ofisi yangu haina taarifa.”

Ujumbe huo uliambatana na picha ya Naibu Waziri Hamis Mwinjuma, maarufu Mwana FA, akiwa amevalia jezi yenye mchanganyiko wa rangi ya njano, bluu, nyeusi na kijani.

Kwa upande wake, Sandaland imesema kauli hiyo imezua taharuki na sintofahamu, huku ikidai kuwa tayari imesababisha madhara ya kiuchumi na kuathiri hadhi ya kampuni.

Kampuni hiyo imeeleza kuwa ina mkataba halali na Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) wa kutengeneza na kusambaza jezi za Taifa Stars, ambazo zimetumika katika mashindano mbalimbali ya timu za taifa za wanaume na wanawake.

Sandaland imeongeza kuwa haitanyamaza na inakusudia kuchukua hatua za kisheria dhidi ya kauli hiyo, ikidai kuwa ilitolewa kwa namna inayoweza kuchafua chapa yake.

Aidha, kampuni hiyo imesisitiza kuwa imejenga jina na heshima yake kwa muda mrefu na imepewa dhamana ya kushughulikia jezi za Taifa Stars.



Na Farida Said Morogoro

Mkuu wa Wilaya ya Kilosa, Mhe. Shaka Hamdu Shaka, leo ameongoza kikao cha Kamati ya Ushauri ya Kodi ya Wilaya kilichofanyika katika Ofisi ya Mkuu wa Wilaya.

Kikao hicho kimejadili tathmini ya mwenendo wa makusanyo ya mapato kwa mwaka wa fedha 2025/2026 na kuweka mikakati ya kuimarisha makusanyo kwa mwaka 2026/2027.Akizungumza katika kikao hicho, Shaka amesema kazi ya kukusanya kodi sio ukusanyaji tu, bali ni ujenzi wa maendeleo.

"Sisi sio wakusanya kodi tu, bali ni wajenzi wa maendeleo. Kila shilingi tunayokusanya kwa haki na uadilifu, tunajenga kesho bora ya wananchi wetu. Hivyo jukumu letu sio dogo," alisema Shaka.

Aidha, Shaka ameelekeza kila chanzo cha mapato Wilayani humo kipitiwe upya.

"Kile ambacho kimekufa kifufue, kile ambacho kinalala kiamshwe. Lazima tubadili mtazamo kutoka kudhibiti kwenda kuelimisha umma," alisisitiza.

Ameitaka TRA na Halmashauri kuimarisha matumizi ya takwimu halisi (Data) na kufunga mihuri yote ya uvujaji wa mapato.

"Mapato yanayokusanywa lazima yaingie yote. Tunahitaji uwazi wa mifumo ya ukusanyaji wa kielektroniki. Wilaya ya Kilosa ina uwezo wa kukusanya zaidi ya mara mbili ya tunayokusanya sasa, kama watendaji wataamua kuwa wabunifu na waadilifu," alifafanua.

Shaka amemalizia kwa kusema, "Tusiogope kufanya mapitio magumu. Bora kuwa na vyanzo 20 hai vinavyoingiza kuliko kuwa na vyanzo 100 hewa vinavyotupa sifa bandia."

Naye Katibu wa kikao hicho, Meneja wa TRA Kilosa, Bi. Saada Mtoto, amesema TRA katika kipindi kilichopita imevuka malengo ya ukusanyaji na kuahidi kufanyia kazi maelekezo yote yaliyotolewa ili kufikia malengo endelevu.






MKURUGENZI wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai, Kamishna wa Polisi Ramadhani Kingai, amegoma kutoa ushahidi kwa upande wa utetezi wa Mwenyekiti wa Chadema, Tundu Lissu, anayekabiliwa na mashtaka ya uhaini katika Mahakama Kuu Masijala Ndogo Dar es Salaam.

Hatua hiyo imempelekea mshtakiwa Lissu, ambaye anajitetea mwenyewe katika kesi hiyo, kufunga ushahidi wa upande wa utetezi.

Kesi hiyo leo, Septemba 18, 2026, iliitwa mahakamani hapo kwa ajili ya kuendelea na ushahidi wa upande wa utetezi, ambapo DCI Kingai alitarajiwa kutoa ushahidi.

Akizungumza mbele ya Jopo la Majaji linaloongozwa na Jaji Dustun Ndunguru, Lissu amedai amekutana na DCI Kingai, ambaye alikuwa amependekeza awe shahidi wake wa leo, ndani ya chumba cha mahakama na kuzungumza naye kwa kina kuhusu suala la kutoa ushahidi kwa upande wa utetezi.

Amedai kuwa baada ya kumweleza Kingai maeneo ambayo angependa ayatolee ushahidi, shahidi huyo alimweleza kuwa hawezi na hayuko tayari kutoa ushahidi kwa upande wa utetezi.

“Mimi nimemuelewa kama hayuko tayari, siwezi kumlazimisha kutoa ushahidi ambao hayupo tayari kuutoa,” amedai Lissu.

Amedai Kingai amemweleza kuwa yeye yuko upande wa watu wanaoomba na watakaoshangilia endapo atapatikana na hatia, hivyo hayuko tayari kutoa ushahidi kwa niaba yake.

“Yeye yuko upande wa wale wanaoomba na watakaoshangilia nikipatikana na hatia, kwa hiyo amesema hayuko tayari kuja kutoa ushahidi kwa niaba yangu,” amedai Lissu.

Amedai Kingai pia amemweleza kuhusu mashahidi wengine wawili ambao ni Mkuu wa Majeshi, CDF Jacob Nkunda, na Mkuu wa Jeshi la Polisi, IGP Camilius Wambura, ambao pia mahakama iliamuru wapelekewe wito, kuwa nao watakaporejea nchini na kupata wito wa mahakama, msimamo wao utakuwa kama wake.

“Kwamba na wao hawatakuwa tayari kutoa ushahidi kwa upande wa utetezi, hawawezi kwa sababu ile ile ya wale wanaoombea na watakaoshangilia nikipatikana na hatia,” amedai Lissu.

Kutokana na hali hiyo, Lissu amesema hana mashahidi wengine wa kuwaita na hivyo ameomba kufunga ushahidi wa upande wa utetezi.

Baada ya kusikiliza maelezo hayo, kesi hiyo sasa imefungwa kwa pande zote mbili na kuomba kupangiwa siku ya kuwasilisha hoja za mwisho.

Upande wa utetezi umeeleza kuwa ratiba ya kikao cha mahakama inaishia Septemba 25, hivyo kubaki siku saba za kuandaa hoja za mwisho.

Lissu amesema yuko tayari kuwasilisha hoja hizo Jumatano, huku akieleza kuwa mwenendo wa kesi una hoja zaidi ya kurasa 1,000.

Upande wa Jamhuri umekubaliana na Lissu kuhusu tarehe hiyo na kueleza kuwa utakuwa tayari kwa ajili ya kuwasilisha hoja za mwisho.

Kesi imeahirishwa hadi Septemba 23, 2026. 



Na Janeth Raphael – MichuziTv

Wakala wa Vipimo (WMA) umewataka wafanyabiashara na wananchi kuacha kutumia madebe, makopo, mafungu na vifaa vingine visivyotambuliwa kisheria kama vipimo katika biashara, ukieleza kuwa matumizi ya vifaa hivyo ni kinyume cha sheria na yanaweza kuchukuliwa kuwa kosa la jinai.

Akizungumza leo jijini Dodoma katika mkutano na waandishi wa habari kuhusu utekelezaji wa majukumu ya Wakala kwa mwaka wa fedha 2025/26 na mwelekeo wa mwaka 2026/27, Afisa Mtendaji Mkuu wa WMA, Alban Kihulla, amesema vipimo visivyo rasmi vinaweza kusababisha bidhaa kupimwa kwa viwango tofauti na hivyo kuwanyima haki watumiaji.

Kihulla amesema matumizi ya madebe na makopo katika kupima bidhaa kwa uzito hayatoi kipimo cha uhakika kwa kuwa kiasi kinachopatikana kinaweza kutofautiana kutoka chombo kimoja hadi kingine, jambo linaloweza kusababisha mfanyabiashara au mlaji kupata kiwango kisicho sahihi cha bidhaa anayolipia.

“Madebe, makopo, visado na mafungu sio vipimo na tumeendelea kutoa elimu kwa wananchi, lakini pia tunaendelea kuchukua hatua dhidi ya wanaojihusisha na upimaji wa aina hiyo,” amesema Kihulla.

Amesema WMA itaendelea kusimamia matumizi ya vipimo sahihi kwa lengo la kuhakikisha biashara zinafanyika kwa haki na kulinda maslahi ya wafanyabiashara pamoja na watumiaji, huku akiwataka wafanyabiashara kuhakikisha wanakuwa na mizani inayokidhi matakwa ya kisheria katika maeneo yao ya biashara.

Aidha, Kihulla amewahimiza wananchi kujenga utamaduni wa kuhakikisha bidhaa wanazonunua zinapimwa kwa mizani sahihi, akisisitiza kuwa matumizi ya vipimo vinavyotambulika kisheria ni sehemu muhimu ya kulinda haki za mlaji na kuhakikisha kila mmoja anapata kiwango cha bidhaa anachostahili.



Na Janeth Raphael - MichuziTv

Wakala wa Vipimo (WMA) umesema jukumu la kuhakikisha vipimo vinavyotumika katika biashara vinafanyika kwa usahihi, pamoja na kutekelezwa kwa mujibu wa sheria, lina msingi pia katika mafundisho yanayopatikana katika vitabu vya dini, ikiwemo Qur’an Tukufu na Biblia Takatifu.

Afisa Mtendaji Mkuu wa WMA, Alban Kihulla, ameyasema hayo leo jijini Dodoma wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu utekelezaji wa majukumu ya Wakala kwa mwaka 2025/26 pamoja na mwelekeo wa utekelezaji kwa mwaka 2026/27.

Kihulla amesema maandiko matakatifu yanasisitiza umuhimu wa kufanya vipimo kwa usahihi, hivyo wafanyabiashara wanapaswa kuhakikisha wanatumia vipimo sahihi na vilivyohakikiwa kwa mujibu wa sheria. Amesema hatua hiyo ni muhimu katika kujenga uadilifu na kuaminiana katika shughuli za biashara.

“Mtu anayetaka kufanya biashara afanye biashara iliyonyooka. Lazima awe na vipimo sahihi na ambavyo vimehakikiwa kwa mujibu wa sheria,” amesema Kihulla.

Amesema WMA, ikiwa ni sehemu ya safari ya kuelekea utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050, itaendelea kuhakikisha vipimo vinavyotumika katika shughuli mbalimbali vinaendana na viwango vinavyotakiwa. “Kilo moja ukipimiwa kweli iwe kilo moja, na si vinginevyo,” amesema.

Kwa mujibu wa Kihulla, usimamizi wa vipimo unalenga kujenga uaminifu katika biashara, kumlinda mlaji pamoja na mtoa huduma, huku ukiisaidia Serikali kupata mapato yanayostahili kupitia matumizi ya vipimo sahihi na vilivyohakikiwa.

Amesema WMA itaendelea kuwa chombo muhimu katika kuwezesha utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050, hususan katika kujenga mazingira ya biashara yenye uaminifu na hatimaye kuchangia ujenzi wa Taifa lenye uchumi imara, jumuishi na wenye ushindani.




NA MWANDISHI WETU, DODOMA

Wananchi na viongozi wa Zanzibar wamepongezwa kwa kufikia muafaka wa kitaifa kwa kuimarisha umoja na mshikamano kuelekea ujenzi wa taifa lenye maendeleo.

Hayo yameelezwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake wa Chama Cha Mapinduzi (UWT) Taifa na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu (MCC), Mary Chatanda, Septemba 18, 2026, Jijini Dodoma.

Chatanda amesema, hakuna shaka kuwa, wananchi na viongozi wa Zanzibar, wamesukumwa na dhamira ya dhati ya ujenzi wa taifa lao badala ya kutanguliza tofauti zao za kisiasa na maslahi binafsi.

"Niwapongeze wananchi na viongozi wa Zanzibar ambao waliangalia maendeleo badala ya tofauti zao za vyama, waliangalia Zanzibar waitakayo yenye neema na ustawi badala ya misuguano isiyokwisha, ndiyo maana wakaona wakae pamoja, waelewane ili kuunganisha nguvu ya pamoja katika kusukuma mbele gurudumu la maendeleo," amesema Chatanda.

Aidha, Chatanda amempongeza Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Dkt. Hussein Mwinyi kwa kuwa na hekima, busara na utulivu huku akiwashirikisha kikamilifu viongozi wastaafu na wengine kutoka vyama vya upinzani katika kutafuta muafaka wa pamoja ili Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK) iundwe na kufanya kazi.

"Rais Dkt. Hussein Mwinyi ameonyesha ukomavu mkubwa wa kiuongozi, kwa kweli nampongeza sana. Vilevile, niwapongeze wanasiasa hasa kutoka Chama cha ACT- Wazalendo, kwa kukubali kukaa meza moja ya mazungumzo ili muafaka upatikane, hatimaye Zanzibar isonge mbele kimaendeleo. Kwa kweli Wazanzibar wamethibitisha kuwa inawezekana kufikia muafaka wa kitaifa kupitia meza ya mazungumzo," amesema.

Ikumbukwe kuwa, tangu kumalizika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba, 2025, kumekuwa na mazungumzo ya pamoja yanayoendelea ili kukamilisha uundwaji wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa baina ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na ACT - Wazalendo.

Septemba 17, 2026, Kamati ya Uongozi ya ACT- Wazalendo, ilikaa kikao maalum kilichofanyika ofisi ndogo za Chama hicho, Vuga Mjini Unguja, ambapo pamoja na mambo mengine, kilifanya uteuzi wa jina la mwanachama anayependekezwa kuwa Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar.

Kufuatia kikao hicho, Septemba 18, 2026, Rais Dkt. Hussein Mwinyi, alifanya uteuzi wa Othman Masoud Othman, kuwa Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, ambapo ataapishwa rasmi Septemba 22, 2026, Ikulu, Zanzibar.

Kukamilika kwa mchakato wa upatikanaji wa Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, kunaendeleza mchakato wa kuteua mawaziri kutoka ACT- Wazalendo ili kukamilisha uundwaji wa serikali ya pamoja ambayo itakuwa chachu ya kuendeleza mipango mizuri ya maendeleo kwa manufaa ya wananchi wa Zanzibar huku umoja, amani, upendo na mshikamano ukiwa nguzo kuu ya maendeleo hayo.


Na Victor Masangu, Kibaha

Mbunge wa viti maalumu Mkoa wa Pwani kupitia chama cha mapoinduzi (CCM) Mariamu Ulega katika kuunga mkono juhudi za seriklai katika kuboresha sekta ya elimu ameahidi kuchangia kiasi cha shilingi milioni 2 kwa ajili ya kuboresha miundombinu katika shule ya msingi ya Mkoani B iliyopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha hususan katika suala la ujenzi wa kujenga uzio.

Akizungumza wakati wa mahafali ya kwanza kwa mchepua wa kiingereza katika shule ya msingi Mkoani B Katibu wa Jumuiya ya umoja wa wanawake (UWT) Mkoa wa Pwani Aziza Hussein kwa niaba ya mgeni rasmi Mbunge wa viti maalumu Mariamu Ulega ambaye pia Mke wa Waziri wa Ujenzi Abdalah Ulega.

Katibu huyo huyo wa UWT Mkoa akitoa salamu za Mbunge huyo amebainisha kwamba anatambua umuhimu mkubwa wa suala zima la elimu hivyo ameamua kuchangia kiasi hicho cha shilingi milioni 2 ambazo zitaweza kusaidia katika mwendelezo wa ujenzi wa uzio katika shule hiyo ya msingi Mkoani B yenye mchepuo wa kiingereza.

"Nashukuru sana nimeweza kushiriki na kualikwa katika mahafali haya ya kwanza katika shule hii ya msingi mkoani B lakini mimi ni Katibu wa UWT Mkoa wa Pwani lakini kwa leo nimepewa heshima ya kipekee kwa ajili ya kuweza kumwakilisha Mbunge wa viti maalumu mheshimiwa Mariamu Ulega ambaye yeye ndiye aliyetakiwa kuwa mgeni rasmi katika sherehe hizi z amahafali,"amebainisha Katibu huyo.

Aidha katibu huyo ameongeza kwamba lengo kubwa ni kuendelea kushirikiana bega kwa bega na walimu, wazazi pamoja na wadau mbali mbali wa maendeleo katika kutoa sapoti na michango yao ambayo itaweza kusaidia katika kukuza sekta ya elimu sambamba na kuboresha zaidi miundombinu katika shule hiyo.

"Mbunge wenu wa viti maalumu mheshimiwa Mariam Ulega ameniagiza kuja kumwakilisha na amesema yupo pamoja nanyi na kwamba amesema kuwa anachangia kiasi cha shilingi milioni mbili na na kuelekeza kwamba fedha hizo zitumike katika kuboresha miundombinu ya ujenzi wa uzio ili watoto hao waweze kusoma katika mazingira ambayo ni rafiki na salama na kwamba ataendelea kuisaidia shule hiyo katika mambo mengine mbali mbali,"ameongeza Katibu huyo.

Katika hatua nyingine amempongeza kwa dhati Rais wa awamu ya sita Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuweza kutenga fedha nyingi ambazo zimeweza kuleta mabadiliko makubwa katika kutekelza miradi ya maendeleo hususan kuboresha sekta ya elimu ikiwemo ujenzi i wa madarasa pamoja na madawati.

Pia katibu huyo mbali na kutoa salamu za mheshimiwa Mbunge wa viti maalumu Mariamu Ulega amesema na wao kama uongozi wa UWT Mkoa wa Pwani wameamua kuchangia kiasi cha shilingi laki tano ikiwa ni moja na jitihada za kuunga mkono juhudi ambazo zinafanywa na Rais Dkt Samia Suluhu Hassan katika kuboresha sekta ya elimu hapa nchini.

Nao baadhi ya wazazi na walezi akiwemo Teodory Joseph pamoja na Joseph Ogutu wameipongeza serikali kwa kuweza kuboresha sekta ya elimu huku wakiiomba kuweka misingi madhubuti ya kuendelea kutenga shule nyingine na kuziingiza katika progamu hiyo ya kuwa na mchepuo wa masomo ya kiingereza.

Mahafali ya kwanza ya kwa mchepuo wa kiingereza katika shule ya Msingi Mkoani B iliyopo Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha Mkoa wa Pwani imeweza kuhudhuliwa na viongozi mbali mbali wa serikali, wazazi na walezi pamoja na wadau wengine mbali mbali wa maendeleo katika sekta ya elimu.



Na Mwandishi Wetu, Tanga.

Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) imewezesha ziara ya mafunzo kwa Viongozi wa Mila (Malaigwanani), Wazee Mashuhuri na kinamama  33 kutoka kata 11 za tarafa ya Ngorongoro kutembelea kiwanda cha kuzalisha na kuchakata mazao ya maziwa cha Tanga Fresh, kilichopo jijini Tanga.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mwenyekiti wa Malaigwanani Ngorongoro na Diwani wa Kata ya Olbalbal, Mhe. Metui Shaudo alisema, ziara hiyo imewapa fursa ya kuona kwa vitendo hatua mbalimbali zinazofanyika katika uchakataji wa maziwa, kuanzia ukusanyaji wa maziwa, uzalishaji na uuzaji wa bidhaa mbalimbali zilizoongezewa thamani.

 “Tumetembelea kiwanda hiki kujifunza na kuona mambo mengi ambayo tunaweza kuyatumia tunaporudi Ngorongoro, tumeona kuwa maziwa yanaweza kuwa na thamani kubwa zaidi yakichakatwa vizuri badala ya kuuzwa yakiwa ghafi kama ambavyo mara nyingi inafanyika kwa wananchi wetu, baada ya ziara hii tutapelekeaa elimu hii kwa wananchi wenzetu ili kuwaongezea tija na kipato kinachotokana na ufugaji,” alisema Mhe. Shaudo 

Kina mama walioshiriki ziara hiyo  wameelezea kufurahishwa na manufaa yanayotokana na  mifugo na kuwaongezea ujuzi wa uchakataji na uongezaji thamani wa mazao ya mifugo na kuahidi kutoa elimu hiyo kwa wananchi wa Ngorongoro ili waendelee kujikwamua kiuchumi.

Kiongozi wa mila kutoka kata ya kakesio Ole Kotika ameeleza kuwa ziara hiyo  inaendelea kuimarisha mahusiano mazuri kati ya hifadhi ya Ngorongoro na wananchi hasa kuwaongezea fursa ya kujifunza shughuli za ufugaji wa kisasa, usindikaji wa bidhaa za maziwa zenye ubora na kuongeza mnyororo wa thamani ambao unasaidia kukuza uchumi wa wananchi.

Ziara ya viongozi hao ni sehemu ya jitihada za Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro kupitia Idara ya Maendeleo ya Jamii ya kuwawezesha wananchi wanaoishi ndani ya hifadhi ya Ngorongoro kupata ujuzi na uzoefu unaoweza kuboresha shughuli zao za kiuchumi na kuongeza thamani ya rasilimali walizonazo.










Na HABIBA MBARUKU, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju amesema kuwa, Haki Jinai si mali ya Taasisi moja bali ni mfumo wenye Taasisi nyingi, wenye lengo la kuhakikisha haki inapatikana mapema ipasavyo kwa usawa, uadilifu na kwa kuzingatia Katiba na Sheria za nchi huku akieleza kuwa wadau wote wanapaswa kushirikiana kwa pamoja ili kuhakikisha haki haicheleweshwi bila sababu za msingi.

Mhe. Masaju ameyasema hayo wakati wa kufunga Mkutano wa Mahakama na Wadau wa Haki Kuhusu Ushirikiano na Mahusiano katika Utekelezaji Majukumu ya Utoaji Haki Mahakamani leo tarehe 17 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

“Haki jinai ni mfumo mmoja wenye taasisi nyingi lakini wenye lengo moja, yaani kuhakikisha kuwa haki inapatikana mapema ipasavyo tunapaswa kuzungumza kuhusu mfumo mzima kwa sababu udhaifu wa kiungo kimoja katika mnyororo wa haki jinai unaweza kuchelewesha haki kwa mfumo mzima,” amesema Jaji Mkuu.

Mhe. Masaju ametoa mfano wa Mtume Paulo anapozungumza kuhusu kanisa ambapo amesema, “ni kama mwili wa binadamu, kama ambavyo kuna mikono, macho, miguu, lakini hivyo vyote ndiyo vinakamilisha mwili. Yaani macho hayawezi kujifanya yenyewe ni bora kuliko mguu na vile viungo vilivyoonekana kama ni dhaifu, hivyo Mungu alivifanya kuwa vya maana zaidi lakini ukweli hapa wote hakuna kiungo dhaifu, hizi Taasisi zote ni muhimu.”

Ameongeza kuwa, jukumu la kwanza la sheria duniani kote ni kusimamia utawala wa sheria, amani na usalama katika jamii na jukumu la pili ni kukusanya kodi kwa ajili ya maendeleo mbalimbali na kuongeza kuwa hata Mwenyezi Mungu huko mbinguni aliweka sheria, na aliyekwenda kinyume na sheria aliwajibika kama ambavyo Lucifer alivyowajibika.

“Kwa hiyo, mkishakuwa zaidi ya mtu mmoja tu lazima mjiwekee sheria namna ya kufanya mambo yenu na kwetu Tanzania utawala wa sheria unapatikana katika Ibara ya 26 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na mfumo wowote lazima uwe unaongozwa na utawala wa sheria, hata Mwenyezi Mungu kule mbinguni aliweka sheria, na bwana mkubwa yule akiitwa Lucifer alipoasi akawajibika” amesema Mhe. Masaju.

Katika hatua nyingine Jaji Mkuu amefafanua kuwa, Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050 inasisitiza juu ya amani, usalama na utulivu, ulinzi wa haki, uhuru wa msingi, uimara wa Taasisi na utawala wa sheria ambao ni kipengele muhimu cha utawala bora kinachosaidia kujenga jamii yenye usawa, uwajibikaji, haki na kuaminiana.

Aidha, ameeleza kuwa, mashauri ya jinai hayaanzii mahakamani wala polisi pekee kwa kuwa vyombo hivyo vyote haviwi sehemu na wakati ambapo matukio hayo ya kihalifu yanatokea hivyo, wadau wote wanapaswa kuungana na kufanya kazi kwa pamoja kama ambavyo viungo katika mwili vinavyofanya kazi kwa pamoja na kutegemeana.

“Kesi ya jinai inaanza kwenye jamii huko tukio linapotokea, inaenda kwenye vyombo vya uchunguzi iwe ni Polisi, ni Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa, ni Mamlaka ya Kuzuia na Kupambana na Dawa za Kulevya, inaenda Ofisi ya Taifa ya Mashtaka, hatimaye kama kuna ushahidi inaenda mahakamani, na waliohusika kumkamata mshukiwa wanakuja kutoa ushahidi mahakamani kama amepatikana na hatia anarudi gerezani kwa ajili ya reform, utaona kwamba huu mnyororo ni mpana ni mnyororo mrefu lakini mnyororo imara, ” ameeleza Mhe. Masaju.

Katika hatua nyingine, amesema kuwa, ni vema kukawa na mtiririko mzuri wa kimfumo wa usimamizi wa mashauri ya jinai ili kuondoa changamoto zinazokwamisha mashauri kumalizika na kuongeza kuwa Mahakama haiwezi kuwa na ufanisi wa asilimia 100, ikiwa hatua zilizotangulia hazifanyi kazi mapema ipasavyo na kwa ufanisi na kwamba kunaweza kuwa na Mahakama yenye uwezo wa kusikiliza Mashauri Majaji na Mahakimu wenye uwezo lakini kama uchunguzi haujakamilika au kuwepo kwa changamoto yoyote shauri haliwezi kuendelea.

“Mahakama haiwezi kuwa na ufanisi wa asilimia 100 ikiwa hatua zilizotangulia Mahakama hazifanyi kazi mapema ipasavyo na kwa ufanisi. Tunaweza kuwa na Mahakama yenye uwezo wa kusikiliza mashauri, Majaji na Mahakimu wenye uwezo, na mifumo ya kielektroniki au miundombinu, lakini pia ni waadilifu. Lakini kama uchunguzi haujakamilika, jalada halijawasilishwa, mashahidi hawapatikani, maelezo hayajakamilika, hati za mashtaka zina kasoro, mshtakiwa hajaletwa mahakamani, au nyaraka muhimu hazijafikishwa mahakamani mapema, katika mtiririko kama huu kesi haiwezi kwenda mbele, hivyo ni vema kukawa na ile systematic flow ya criminal justice ya case management ili kuondoa hizo changamoto” amesisitiza Jaji Mkuu.

Akizungumza kuhusu uwajibikaji na kujituma, Mhe. Masaju amesema kuwa, kila Taasisi ya Haki Jinai inapaswa kuwajibika ipasavyo ili kuondoa ucheleweshaji wa mashauri bila kusubiri shauri lifike mahakamani huku akirejea Ibara ya 25 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo inasisitiza juu ya uwajibikaji na kujituma katika kila kazi kwa kufahamu chanzo cha kukwama kwa shauri, wapi lilipofikia katika utekelezaji, imefikia hatua zipi za ushahidi, jambo litakalosaidia mnyororo mzima wa haki jinai kufanya kazi vizuri.

Kadhalika, Mhe. Masaju amewakumbusha wadau wa Haki Jinai kwamba, mfumo unahitaji ushirikiano thabiti, mawasiliano ya karibu na uratibu mzuri ambayo ndio nguzo ya mafanikio hivyo, taasisi zote zifanye kazi bila kujitenga.

“Ni vyema tukumbuke kuwa, mfumo wetu wa haki jinai unahitaji ushirikiano thabiti (cooperation), mawasiliano ya karibu (communication), na uratibu mzuri (coordination). Hivi vitu vitatu yaani Cooperation, Communication, and Coordination ndivyo nguzo kuu za mafanikio yetu katika usimamizi wa haki jinai. Kama taasisi moja inafanya kazi kwa kujitenga au bila kutoa taarifa kwa nyingine, ni wazi kuwa, kutakuwa na kukwama kwa mashauri au kuchelewa kwa haki,” amesisitiza Jaji Mkuu.

Kadhalika, Mhe. Masaju amezitaka Taasisi za mnyororo wa Haki Jinai kuzingatia matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) na kuhakikisha mifumo inasomana ili kurahisisha mchakato mzima wa kuhakikisha haki inapatikana mapema ipasavyo bila kucheleweshwa na sababu zisizo na msingi.

Akihitimisha hotuba yake. Mhe. Masaju amezitaka Taasisi za mnyororo wa Haki Jinai kuchukua tahadhari juu ya uwepo wa mvua za El nino kwa kuhakikisha wanaweka miundombinu imara itakayowawezesha kufanya kazi pindi mvua hizo zitakapoanza kunyesha.
Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Majaji, Viongozi na Watumishi wa Mahakama pamoja na Wadau wa Haki Jinai wakati wa Mkutano wa Mahakama na Wadau wa Haki Kuhusu Ushirikiano na Mahusiano katika Utekelezaji Majukumu ya Utoaji Haki Mahakamani uliofanyika tarehe 17 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Aliyeketi kushoto ni Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Amir Mruma na kulia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akitoa hotuba ya kufunga Mkutano wa Mahakama na Wadau wa Haki Kuhusu Ushirikiano na Mahusiano katika Utekelezaji Majukumu ya Utoaji Haki Mahakamani uliofanyika tarehe 17 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.





Baadhi ya Viongozi, Watumishi wa Mahakama pamoja na Wadau wa Haki Jinai wakisikiliza hotuba ya Jaji Mkuu alipokuwa akifunga Mkutano wa Mahakama na Wadau wa Haki Kuhusu Ushirikiano na Mahusiano katika Utekelezaji Majukumu ya Utoaji Haki Mahakamani uliofanyika tarehe 17 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Amir Mruma akitoa neno wakati wa kufunga Mkutano wa Mahakama na Wadau wa Haki Kuhusu Ushirikiano na Mahusiano katika Utekelezaji Majukumu ya Utoaji Haki Mahakamani uliofanyika tarehe 17 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya akitoa taarifa ya utekelezaji wa mikakati kwa upande wa Mahakama wakati wa Mkutano kati ya Mahakama na Wadau wa Haki Kuhusu Ushirikiano na Mahusiano katika Utekelezaji Majukumu ya Utoaji Haki Mahakamani uliofanyika tarehe 17 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


(Picha na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo imesema haitambui matamko yanayohusu jezi mpya za timu za taifa, ikieleza kuwa mchakato wa kubadilisha jezi hizo haukuishirikisha Wizara licha ya maelekezo yaliyotolewa mwezi Februari 2026.

Kwa mujibu wa taarifa kwa umma iliyotolewa na Wizara hiyo leo September 18, 2026 imesema Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Christian Makonda, ameeleza kuwa Serikali inawekeza fedha nyingi katika maandalizi ya timu za taifa zinazoshiriki mashindano ya kimataifa.

Taarifa hiyo imeongeza kuwa, kwa kuzingatia Tanzania kuwa mwenyeji wa mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2027, kuna umuhimu wa kuboresha jezi za timu za taifa ili ziakisi manufaa mapana kwa nchi.

Aidha, Wizara imesema Waziri Makonda ataandaa Kamati ya kuchunguza mkataba wa mzabuni wa jezi za timu za taifa, kwa lengo la kubaini manufaa yanayotokana na mkataba huo kwa timu hizo.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, hatua hiyo inazingatia ukweli kwamba Serikali imekuwa ikitumia fedha nyingi kuendesha timu za taifa, huku kukiwa na fursa ya mauzo ya jezi ambazo zinaweza kuchangia katika uendeshaji wa timu hizo.





 Na Mwandishi Wetu, Arusha

HOSPITALI ya JKCI–ALMC Arusha (Selian ya Mjini) imeandaa Kambi Maalum ya Matibabu ya Kibingwa itakayofanyika kuanzia Septemba 21 hadi 24, 2026, ikiwakutanisha madaktari bingwa na wabobezi kutoka Tanzania na India.

Mkurugenzi wa Hospitali hiyo, Dkt. Tatizo Waane, alisema jana kuwa kambi hiyo itawakutanisha wataalamu kutoka Apollo Hospitals–India, Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Taasisi ya Mifupa Muhimbili (MOI), Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH) pamoja na madaktari bingwa wa JKCI–ALMC Arusha.

Dkt. Juma Magogo Mzimbiri,, Daktari Bingwa wa Upasuaji wa Ubongo, Uti wa Mgongo na Mfumo wa Fahamu kutoka MOI,

Alisema kambi hiyo imelenga kuwafikishia wananchi huduma za kibingwa katika maeneo ya magonjwa ya mfumo wa fahamu, upasuaji wa ubongo na uti wa mgongo, magonjwa na upasuaji wa mfumo wa mkojo, pamoja na magonjwa, upasuaji wa mifupa, viungo na majeraha.

“Tunatarajia kuona wagonjwa kati ya 100 hadi 200 kwa siku. Watapata nafasi ya kuonana na madaktari bingwa, kufanyiwa tathmini, kupata ushauri wa kitaalamu na kuelekezwa kuhusu hatua zinazofaa za matibabu,” alisema Dkt. Waane.

Dkt. Mahendra Pal, Daktari Bingwa wa Saratani za Mfumo wa Mkojo (Uro-Oncology) kutoka Apollo Hospitals, Mumbai, India.

Alisema huduma zitakazotolewa moja kwa moja kupitia kambi hiyo zitakuwa bila malipo, lakini mgonjwa atakayehitaji vipimo, dawa, upasuaji au huduma nyingine za ziada atachangia gharama kulingana na huduma inayohitajika.

Kwa mujibu wa Dkt. Waane, baadhi ya wagonjwa watakaobainika kuwa na matatizo yanayohitaji matibabu ya kina wataandaliwa kwa ajili ya upasuaji au huduma nyingine za kibingwa kulingana na tathmini ya madaktari. Alitoa wito kwa wananchi wa Arusha na mikoa jirani, ikiwemo Kilimanjaro, Manyara, Singida na maeneo mengine ya Kanda ya Kaskazini, kutumia fursa hiyo.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Tiba wa JKCI–ALMC Arusha na Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo, Dkt. Salehe Hamisi Mchete, alisema kambi hiyo ni sehemu ya juhudi za kusogeza huduma za kibingwa na ubingwa bobezi karibu zaidi na wananchi.

Alisema pamoja na kutoa huduma kwa wagonjwa, kambi hiyo itatumika kujenga uwezo wa wataalamu wa afya kupitia Mafunzo Endelevu ya Kitabibu (CME) yatakayoshirikisha madaktari bingwa kutoka Tanzania na India.

“Tunataka baada ya kambi hii wagonjwa wapate huduma, lakini pia maarifa yabaki kwa wataalamu wetu. Tutajadili mbinu za kisasa za matibabu, teknolojia mpya za upasuaji na namna bora zaidi ya kuwahudumia wagonjwa,” alisema Dkt. Mchete.

Akizungumza kwa niaba ya timu ya madaktari kutoka Apollo Hospitals–India, Dkt. Mahendra Pal, Daktari Bingwa wa Saratani za Mfumo wa Mkojo (Uro-Oncology), alisema wamefurahishwa kupata nafasi ya kuja Tanzania kufanya kazi pamoja na madaktari bingwa wa hapa nchini.

Dkt. Pal, ambaye amebobea katika saratani za tezi dume, figo, kibofu cha mkojo, korodani na saratani nyingine za mfumo wa mkojo, alisema wataalamu kutoka Apollo watashirikiana na madaktari wa Tanzania katika maeneo ya urology, neurosurgery na orthopaedics.



“Tunafurahi kuja Tanzania na kufanya kazi pamoja na wataalamu wa hapa. Tunawaalika wananchi kutumia fursa hii kuonana na madaktari waliobobea na kupata huduma zinazohitajika,” amesema.

Daktari Bingwa wa Upasuaji wa Ubongo, Uti wa Mgongo na Mfumo wa Fahamu kutoka MOI, Dkt. Juma Magogo Mzimbiri, alisema ujio wa wataalamu hao ni fursa muhimu kwa wananchi wa Arusha na Kanda ya Kaskazini kupata huduma za madaktari bingwa wa ndani na nje ya nchi katika eneo moja.

Amesema katika kambi hiyo atashiriki pamoja na Dkt. Remigius Rugakingira, Daktari Bingwa wa Mfumo wa Mkojo kutoka BMH, na Dkt. Emil Urasa, Daktari Bingwa wa Upasuaji wa Mifupa na Majeraha kutoka MOI.

“Tunawahimiza wananchi wenye matatizo ya uti wa mgongo, ubongo, kifafa, kiharusi na matatizo mengine ya mfumo wa fahamu kutumia fursa hii. Vilevile wenye matatizo ya mfumo wa mkojo, tezi dume, matatizo ya korodani kwa watoto na baadhi ya changamoto za figo zinazohitaji tathmini ya urology wanakaribishwa,” amesema Dkt. Magogo.


Uongozi wa JKCI–ALMC Arusha (Selian ya Mjini) umetoa wito kwa hospitali na vituo vya afya kuwaelekeza wagonjwa wanaoweza kunufaika na huduma hizo, huku taasisi za afya zikihimizwa kuwawezesha wataalamu wao kushiriki katika mafunzo ya CME.

Kambi hiyo itafanyika JKCI–ALMC Arusha (Selian ya Mjini) kuanzia Septemba 21 hadi 24, 2026.

Na. Philipo Hassan - Mikumi

Ujenzi wa uwanja wa ndege wa Kikoboga uliopo ndani ya Hifadhi ya Taifa Mikumi umefikia asilimia 75, ukihusisha jengo lenye uwezo wa kuhudumia abiria 160 kwa ujumla wanaowasili na wanaoondoka, njia ya kurushia na kutua ndege (Runway) yenye urefu wa kilomita 1.8, jengo la Kikosi cha Zimamoto na Uokoaji, sehemu ya maegesho ya ndege na magari pamoja na kioski. 

Kukamilika kwa uwanja huo kunatarajiwa kuongeza idadi ya watalii, kukuza mapato kwa Taifa na kuchochea shughuli za kiuchumi kwa jamii inayozunguka hifadhi.

Akikagua mradi huo jana Septemba 17, 2026, Kamishna wa Uhifadhi, Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) Massana Mwishawa amemwelekeza mkandarasi “China Henan International Cooperation, Group Co. LTD (CHICO)” kuhakikisha mradi huo unakamilika kwa wakati na kwa viwango vilivyokusudiwa ili kuleta tija kwa Taifa na jamii. Aidha, ameitaka Menejimenti ya Hifadhi kusimamia miradi hiyo kwa ufanisi sambamba na kuimarisha utekelezaji wa shughuli za uhifadhi na utalii.

Pia, Kamishna Mwishawa alifanya ukaguzi wa ujenzi wa barabara inayotokea lango la Kikoboga hadi lango la Chamgore yenye urefu wa kilometa 38, ambayo ukarabati wake umefikia asilimia 80. Ujenzi wa barabara hiyo unatekelezwa chini ya ufadhili wa fedha za Mfuko wa Kukuza Utalii nchini (TDL) unaosimamiwa na Wizara ya Maliasili na Utalii na kutekelezwa na TANAPA.

Barabara hiyo itaunganisha Lango la Chamgore lililopo upande wa Kilosa linalotarajiwa kuanza kujengwa mwaka huu, hivyo itaongeza wigo mkubwa wa mtandao wa njia za utalii ndani ya hifadhi kwa kuwawezesha watalii watakokuwa wanashuka na treni ya mwendo kazi (SGR) mjini Kilosa na kuingia hifadhini.

Hifadhi ya Taifa Mikumi ni miongoni mwa hifadhi zinazovutia katika ukanda wa mashariki mwa Tanzania, ikifahamika kwa urahisi wa kufikika na fursa ya kuona wanyamapori kwa haraka. Miongoni mwa vivutio vyake ni pamoja na makundi ya tembo, nyati, simba na twiga, pamoja na mandhari ya kuvutia na fursa nzuri ya kufanya utalii wa ndege.










Na Mwandishi Wetu

KAMPUNI ya Oryx Gas imekabidhi mitungi ya gesi 600 na vifaa vyake kwa wananchi wa Wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kampuni hiyo kuhakikisha Watanzania wengi zaidi wanapata fursa ya kutumia nishati safi, salama na rafiki kwa mazingira.

Oryx Gas imetoa mitungi hiyo ya gesi kwa wananchi hao kwa kushirikiana na Mbunge wa Jimbo la Namtumbo mkoani Ruvuma ambaye pia ni Waziri wa Katiba na Sheria Juma Homera kwa lengo la kuendelea kuhamasisha matumizi ya nishati safi nchini ili kulinda mazingira na kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa Oryx Gas Tanzania Iman Mtafya,Meneja Fedha wa kampuni hiyo Ashery Mbasha amesema kupitia Uwezeshaji huo Oryx Gas inaendelea kuunga mkono juhudi za Serikali za kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini.

“Wilaya ya Namtumbo, kama ilivyo kwa maeneo mengi nchini Tanzania, imekuwa ikikabiliwa na changamoto ya matumizi makubwa ya kuni na mkaa. Hali hii imechangia kwa kiasi kikubwa ukataji wa miti na uharibifu wa mazingira.

“Hivyo kamahatua madhubuti hazitachukuliwa, vizazi vijavyo vinaweza kukumbana na uhaba mkubwa wa rasilimali za misitu na athari za mabadiliko ya tabianchi,”amesema na kuongeza kwa kutambua changamoto hiyo, Oryx Gas imeamua kuwa sehemu ya suluhisho kwa kuhamasisha matumizi ya gesi ya LPG kama mbadala wa kuni na mkaa.

Amesisitiza matumizi ya gesi ya kupikia yatasaidia kupunguza kasi ya ukataji miti, kuboresha afya za wananchi kwa kupunguza moshi majumbani, kuokoa muda wa kupika na kuongeza ubora wa maisha kwa ujumla.

Mbasha amesema dhamira ya Oryx Gas ni kuhakikisha Tanzania inafikia mabadiliko kamili ya matumizi ya nishati safi ya kupikia. Wilaya ya Namtumbo ni moja ya maeneo ambayo tumeyawekea kipaumbele katika safari hii muhimu.

“Oryx Gas pia imekuwa mshirika wa maendeleo katika wilaya hii ya Namtumbo kupitia miradi mbalimbali ya nishati safi. Miongoni mwa mafanikio hayo ni ufungaji wa mfumo wa hifadhi na usambazaji wa gesi ya LPG katika Shule ya Wasichana ya Samia Suluhu, hatua iliyowezesha taasisi hiyo kutumia nishati safi kwa manufaa ya wanafunzi na watumishi wake.”

Ametumia nafasi hiyo kutoa rai kwa wananchi wa Namtumbo hasa waliopata mitungi ya gesi ya Oryx kutumia majiko hayo kwa usalama na kuendelea kueneza elimu ya matumizi ya gesi ya LPG katika jamii zenu. Kwa pamoja tunaweza kujenga Namtumbo yenye mazingira bora, afya bora na maendeleo endelevu.

Awali akizungumza kwenye hafla hiyo Mbunge wa Jimbo la Namtumbo ,ambaye pia ni waziri wa Katiba na sheria Dk.Juma Homera ameishukuru kampuni ya Oryx kwa kuwapatia majiko 600 na Kati hayo majiko 215 yamekabidhiwa kwa wananchi wa Namtumbo na mengine yatapelekwa na kugawanywa kila kata kwa wananchi wa Wilaya hiyo.

Dk.Homera amesema Rais Dk.Samia Suluhu Hassan ambaye ni kinara wa nishati safi ya kupikia amekuwa akisisitiza utumiaji wa nishati safi hivyo amewataka wananchi kuunga mkono jitihada hizo za Rais na Serikali ya Awamu ya Sita kwa vitendo huku akiipongeza Oryx gas kwa ushirikiano ambao wamekuwa wakiutoa kwa wananchi wa Namtumbo.

Kwa upande wake Mama Lishe Anifa Mahela amepongeza mpango huo mzuri wa kutoa elimu na kugawa bure mitungi kwa wajasiriamali huku akiiomba Serikali na wadau kama Oryx kuwasaidia kupata mitungi ya gesi na majiko ya nishati safi kwa bei ya ruzuku kutokana na mtaji mdogo walionao.









Top News