Na: Mwandishi Wetu, DAR

Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) imeanza rasmi kupokea maombi ya mikopo kwa wanafunzi wa elimu ngazi ya Stashahada (Diploma) katika kozi za vipaumbele wanaotarajiwa kudahiliwa mwezi Machi, 2026.

Hayo yameelezwa na Mkurugenzi Mtendaji wa HESLB, Dk. Bill Kiwia, Jijini Dar es Salaam ambapo dirisha la maombi ya mikopo hiyo limefunguliwa Februari 15, 2026 hadi Machi 15, 2026. 

"Niwahimize wale wote wanaotarajiwa kudahiliwa mwezi Machi, 2026, katika kozi za vipaumbele kutumia vyema dirisha hili la uombaji mikopo ili waweze kutimiza malengo yao ya kielimu," amesema Dk. Kiwia.

Katika hatua nyingine, Dk. Kiwia amewasisitiza waombaji wote kusoma vyema mwongozo wa utoaji mikopo kwa wanafunzi wa ngazi ya Stashahada unaopatikana katika tovuti ya Bodi ya Mikopo ili kuzingatia vigezo muhimu vilivyoainishwa.

Kimsingi, serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan imeweka mkazo wa kuhakikisha vijana wa Kitanzania wanapata elimu bila vikwazo ambapo elimu ya Awali hadi Kidato cha Sita inatolewa bila ada. 

Kwa upande wa elimu ya kati na Ile ya ngazi ya Stashahada katika kozi za vipaumbele na kozi nyingine za Shahada, serikali kupitia HESLB inatoa mikopo ili kuwawezesha vijana wengi zaidi hasa wanaotoka familia zenye changamoto za kiuchumi kupata mikopo hiyo ya elimu kwa ustawi wa maisha yao.

Na Fatma Jalala

Elimu na ushiriki wa wanawake katika ununuzi wa umma ni mhimili muhimu wa kukuza maendeleo ya kiuchumi na kujenga uchumi jumuishi nchini Tanzania, hasa katika kipindi hiki ambacho Serikali inaendelea kutekeleza Sheria ya Ununuzi wa Umma ya mwaka 2023.

Sheria hiyo inazitaka taasisi zote za umma kutenga asilimia 30 ya ununuzi kwa ajili ya makundi maalum yanayohusisha wanawake, vijana, watu wenye ulemavu na wazee.

Hata hivyo, wanawake wajasiriamali na vikundi vya wanawake katika maeneo ya mijini na vijijini, ikiwemo wilaya ya Kinondoni, bado wanakabiliwa na changamoto ya uelewa mdogo wa taratibu za kushiriki katika zabuni za Serikali.

Kwa mujibu wa taarifa za Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA) ya mwaka 2025, kati ya shilingi trilioni 14.9 zilizotumika kufanya ununuzi wa umma kupitia mfumo wa NeST, ni takribani shilingi bilioni 15 pekee zilikwenda kwa makundi maalum yote, kiwango ambacho ni chini ya asilimia moja ya thamani ya ununuzi wa umma.

Takwimu hizi zinaonyesha pengo kubwa kati ya malengo ya sera na utekelezaji halisi wa fursa kwa makundi maalum.

Ununuzi wa umma ni moja ya nguzo kuu za utekelezaji wa bajeti ya Serikali na chombo muhimu cha kuchochea uchumi. Kila mwaka Serikali hutumia zaidi ya asilimia 70 ya bajeti yake kufanya ununuzi wa bidhaa na huduma.

Ili fedha hizi ziwanufaishe na watu wa ngazi za chini pia, Serikali iliweka utaratibu wa kutenga angalau asilimia 30 ya thamani ya ununuzi wa umma kwa makundi maalum.

Lakini utafiti mbalimbali umeonyesha changamoto katika utekelezaji wa fursa hii. Kwa mfano, ripoti ya Africa Freedom of Information Centre (AFIC) kuhusu ununuzi jumuishi imeonyesha kuwa licha ya wanawake kumiliki sehemu kubwa ya biashara ndogo na za kati nchini, bado wanapata sehemu ndogo sana ya zabuni za Serikali kutokana na changamoto za uelewa mdogo wa taratibu za zabuni, urasimu na ukosefu wa taarifa sahihi.

Elimu ni kizuizi

Katika mahojiano na wanawake wajasiriamali wa Kinondoni, wengi walikiri kutokuwa na uelewa kuhusu fursa za ununuzi wa umma.

Blandina Daniel, mama lishe katika soko la Tandale, anasema: "Wanawake wengi hawajawahi kupata elimu kuhusu mfumo wa NeST wala ununuzi wa umma.”

Theresia Paschal Joseph, mjasiriamali katika soko la Magomeni, anasema: "Maisha ya ujasiriamali yamekuwa yakitegemea mapato ya kila siku bila matarajio ya kupanua biashara kutokana na kukosa taarifa na fursa."

Ingawa baadhi yao wanasema wamewahi kusikia juu ya fursa ya asilimia 30 kupitia vyombo vya habari, lakini hawajui hatua za kufuata ili kushiriki kikamilifu na wengi wao hawajasikia kabisa.

Kwa mujibu wa taarifa zilizowahi kutolewa wakati wa makubaliano ya ushirikiano kati ya PPRA na Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (NEEC) mwaka 2024, changamoto ya ukosefu wa uelewa na elimu ya ununuzi wa umma imekuwa moja ya sababu kuu zinazokwamisha makundi maalum kunufaika na fursa hizi.

Wanawake wengi wanahitaji mafunzo ya vitendo yanayohusisha namna ya kuunda vikundi halali, kupata vyeti vya usajili, kuandaa nyaraka za zabuni na kutumia mifumo ya kielektroniki kama NeST.

Viongozi wa mitaa wakiri pengo la elimu

Baadhi ya viongozi wa Serikali za Mitaa akiwemo Mwenyekiti wa Serikali za Mitaa Salum Kaponda wamekiri kuwa elimu kuhusu mfumo wa ununuzi wa umma bado haijawafikia wananchi kwa kiwango kinachohitajika.

Hali hii inaathiri uwezo wa wanawake kupata taarifa sahihi kuhusu fursa zilizopo.

Naye Diwani wa Kata ya Tandale, Abdulaziz Said, anasema hajawahi kupata taarifa rasmi kuhusu elimu ya mfumo huo.

Utafiti wa Africa Freedom of Information Centre (AFIC) ukiungwa mkono na PPRA, unaonyesha kuwa licha ya sheria ya Ununuzi wa Umma kutaka taasisi za umma kutenga asilimia 30 ya bajeti ya ununuzi kwa makundi maalum, utekelezaji wake umekuwa mdogo sana.

Watafiti walibaini kuwa taasisi nyingi hazitii kikamilifu masharti hayo. Kwa mfano, bajeti ya mwaka 2021 baadhi ya taasisi hazikutenga kabisa bajeti ya ununuzi wa umma kwa ajili ya makundi haya.

Wajasiriamali wenyewe wanasema hali hii inasababishwa na mambo kadhaa ikiwemo ukosefu wa uelewa wa sheria, taratibu tata za usajili wa makundi katika mfumo wa NeST, na kutokuwepo kwa data ya kutosha juu ya utekelezaji wa sera hizi katika ngazi mbalimbali za serikali.

Kwa mujibu wa ripoti za hivi karibuni kutoka PPRA hadi mwisho wa mwaka 2024, jumla ya makundi maalum 210 yalifanikiwa kushinda zabuni kupitia mfumo wa NeST, ikiwa na thamani ya takriban shilingi bilioni 9.85.

Katika hayo, vikundi vya wanawake vilishinda zabuni zenye thamani ya takriban shilingi bilioni 4 tu, na vikundi vya vijana vilishinda zabuni zenye thamani ya shilingi bilioni 3.9.

Hata hivyo, ingawa hizi ni takwimu chanya ikilinganishwa na hali ya awali, kiwango cha utekelezaji bado hakifikii kikomo cha asilimia 30 kinachotakiwa na sheria jambo linalobainika kuwa changamoto ya utekelezaji wa sera zinazolenga makundi maalum.

Kwa kifupi, uchambuzi huo unaonyesha kuwa ingawa serikali imeanzisha sheria ya ununuzi wa umma na mikakati kama makubaliano ya PPRA na NEEC, utekelezaji na ushiriki wa makundi maalum hasa wanawake bado unakabiliwa na vikwazo.

Makubaliano kati ya PPRA na Baraza la Taifa la Uwezeshaji Uchumi (NEEC) yalisainiwa mwaka 2024 ili kuboresha uelewa na uwezo wa makundi maalum kushiriki kikamilifu katika zabuni za serikali. Sheria ya ununuzi inataka asilimia 30 ya zabuni ziwe kwa makundi kama wanawake, vijana, watu wenye ulemavu na wazee.

Hata hivyo, data ya utafiti inaonyesha kuwa utekelezaji umekuwa hafifu, taasisi nyingi bado hazitii kikamilifu vipaumbele vya asilimia 30, na sababu kubwa ni ukosefu wa uelewa wa taratibu za zabuni, ukosefu wa data bora ya makundi maalum, pamoja na kanuni tata za usajili za makundi katika mfumo wa NeST. Pia, sheria hiyo inahitaji makundi kuwa na muundo maalum wa kikundi, jambo lililozua usumbufu kwa wafanyabiashara binafsi wakiwemo wanawake wanaoishi maeneo tofauti na wenye biashara za mtu mmoja.

Umuhimu wa ushiriki wa wanawake

Wataalamu wa uchumi wanaeleza kuwa ushiriki wa wanawake katika ununuzi wa umma una faida kubwa kwa uchumi wa taifa.

Unasaidia kuongeza kipato cha wanawake na familia zao, kupunguza umasikini wa kaya, kukuza ujasiriamali na kuongeza pato la Taifa kupitia kodi.

Wanawake wengi wana ujuzi na ubunifu mkubwa wa kuzalisha bidhaa na huduma bora kwa gharama nafuu. Kupitia ununuzi wa umma, wanaweza kupata soko la uhakika na kukuza biashara zao kwa kiwango kikubwa zaidi.

Ili kuongeza ushiriki wa wanawake katika ununuzi wa umma, ni muhimu kuimarisha utoaji wa elimu na mafunzo ya vitendo kuhusu taratibu za zabuni, usajili wa biashara na vikundi, matumizi ya mfumo wa NeST, na ushirikiano wa taasisi husika.

Wanawake wanapaswa kuunda vikundi halali au kusajili biashara zao, kusajili kampuni kupitia BRELA, kujiunga na vyama vya ushirika au SACCOS, pamoja na kujisajili katika mfumo wa NeST. Ni muhimu pia kuwa na nyaraka halali kama cheti cha usajili, TIN na akaunti ya benki ya kikundi au biashara

Pamoja na uwepo wa sheria na sera rafiki, bado kuna haja ya kuongeza elimu na uhamasishaji kwa wanawake ili waweze kushiriki kikamilifu katika ununuzi wa umma.

Ushirikishwaji wa wanawake katika ununuzi wa umma si hisani, bali ni haki ya kisheria na mkakati muhimu wa maendeleo ya Taifa.

Kama watajengewa uwezo kupitia elimu sahihi, mafunzo ya vitendo na ushirikiano wa taasisi husika, wanawake wana uwezo mkubwa wa kuchangia ukuaji wa uchumi wa taifa na kuboresha maisha ya familia na jamii kwa ujumla.

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu tarehe 14 Februari 2026 imetembelea Chuo cha Bahari Dar es Salaam (DMI) kwa ziara ya kikazi yenye lengo la kujua shughuli zinazofanywa na Chuo katika utekelezaji wa majukumu yake ya kitaifa.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mwenyekiti wa Kamati Mhe. Moshi Kakoso aliipongeza menejimenti na watumishi wa DMI kwa juhudi kubwa katika kuzalisha wataalamu wanaochangia katika sekta ya bahari na usafiri wa majini. Aliahidi kuchukua hatua kuhusu changamoto na maoni yaliyotolewa na wajumbe wa Kamati na wabunge wengine ili kuhakikisha chuo kinaendelea kustawi na kufikia malengo yake ya kimkakati.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Uchukuzi Mhe. David Kihenzile alibainisha kuwa Serikali ya Awamu ya Sita imejikita katika kuboresha sekta ya usafiri wa majini kupitia ujenzi, ukarabati, na upanuzi wa bandari. Amesema jitihada hizo zinategemea nguvu kazi yenye ujuzi mkubwa, na kwamba DMI ni kitovu cha kuzalisha wataalamu watakaoiwezesha sekta hiyo kukua kwa kasi.

Akizungumzia kuhusu Uchumi wa Buluu, Naibu Waziri alisema Serikali inaendeleza matumizi endelevu ya rasilimali za bahari na maziwa makuu kwa ajili ya kukuza uchumi wa taifa. Alisisitiza kuwa DMI ina wajibu wa kuzalisha wataalamu, kufanya tafiti, na kutoa ushauri wa kitaalamu utakaosaidia nchi kunufaika zaidi na rasilimali hizo. Aidha, aliongeza kuwa mafanikio ya sekta ya bahari na rasilimali za majini yanategemea kwa kiasi kikubwa wataalamu wanaotoka DMI.
Mkuu wa Chuo, Prof. Tumaini Gurumo, katika taarifa yake alieleza kuwa licha ya mafanikio yaliyopatikana, bado kuna uhitaji wa kuboresha miundombinu ya kufundishia na kujifunzia, pamoja na kuendelea kuwasomesha waalimu nje ya nchi.



Aliongeza kuwa chuo katika kuliona hilo kimeanza kutekeleza mpango wa upanuzi wa huduma zake katika Mikoa ya Dar es Salaam, Pwani, Lindi, Mwanza, Simiyu na Pemba ili kukidhi mahitaji ya elimu na mafunzo ya bahari.

Alibainisha kuwa DMI inaendelea kunufaika kupitia ushirikiano na taasisi mbalimbali za kimataifa na sekta binafsi, ambao huchukua wanafunzi na kuwapa mafunzo kwa vitendo kwa kutumia meli zao na kubadilishana uzoefu wa kitaaluma.

Prof. Gurumo vilevile aliishukuru Serikali kwa kuendelea kukiwezesha chuo kutimiza majuku yake ikiwa ni pamoja na kukipatia vifaa vya kisasa vya kufundishia kama vile mitambo ya kisasa ya mafunzo kwa vitendo (simulators), ambavyo vimeongeza ubora wa mafunzo unaoendana na maendeleo ya teknolojia ya usafiri wa majini.

Wajumbe wa Kamati walikipongeza chuo kwa mchango wake katika kukuza sekta ya bahari na kusema kuwa wameona umuhimu wa chuo hicho kuwezeshwa kwa miundombinu bora, meli ya mafunzo na vifaa vya kisasa ili kuimarisha uzalishaji wa wataalamu kwa maendeleo ya Uchumi wa Buluu.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwasili Kiwanja che Ndege cha Kimataifa cha Abeid Amani Karume, Zanzibar na kupokelewa na Viongozi mbalimbali akitokea nchini Ethiopia baada ya kukamilisha ziara ya kikazi ya siku nne, ambapo pamoja na mambo mengine alishiriki Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika (AU) uliofanyika tarehe 14 na 15 Februari, 2026.

Na Mwandishi wetu, Simanjiro
MADIWANI wa halmashauri ya wilaya ya Simanjiro mkoani Manyara, wamepitisha kiasi cha 45,136,269,016.60 kwa ajili ya rasimu wa mpango wa bajeti kwa mwaka wa fedha wa 2026/2027.

Afisa mipango wa Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro, Happy Masatu akisoma mpango huo wa makisio ya bajeti leo amesema umelenga kufanikisha miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo ya elimu, afya, maendeleo ya jamii, kilimo na mifugo.

Amesema mpango huo wa rasimu ya bajeti ya mwaka wa fedha wa 2026/2027 umeandaliwa kwa kuzingatia sheria, sera, mikakati ya halmashauri na miongozo ya kiserikali.

"Mpango umelenga muongozo wa maandalizi ya mpango wa bajeti ya serikali kwa mwaka 2026/2027, hotuba ya Rais Samia Suluhu Hassan akifungua Bunge la 13, ilani ya uchaguzi ya chama cha mapinduzi (CCM) na vipaumbele vya halmashauri," amesema Masatu.

Amesema mapato ya ndani ya halmashauri hiyo yameongezeka maeneo ya ushuru wa mchanga, mazao ya biashara na chakula, minada, masoko, stand ya magari, kodi ya huduma, ushuru wa trekta na uuzaji wa viwanja.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Simanjiro, Kaleiya Melita Mollel ameeleza kwamba madiwani washirikiane na watumishi wa halmashauri katika kuteketeza miradi mbalimbali ya maendeleo.

"Watu kule kwenye kata zetu wanamatarajio makubwa katika kupata huduma za umuhimu kupitia bajeti ya mwaka huu kwenye sekta ya afya, elimu, maji, miundombinu ya barabara na mengineyo," amesema Mollel.

Kaimu Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro, Dominika Ngaleka amewashukuru madiwani hao kwa kupitisha mpango huo wa bajeti kwa mwaka wa fedha wa 2026/2027.

"Tunatarajia watumishi wa halmashauri watashirikiana na madiwani wetu ili kuhakikisha utekelezaji wa mpango wa bajeti ya mwaka wa fedha wa 2026/2027 unatekelezeka ipasavyo," amesema Ngaleka.

Kaimu Katibu Tawala wa Wilaya ya Simanjiro Tumaini Sebastian, ameeleza kwamba ofisi ya DC inaelekeza suala la changamoto ya madawati, viti na meza katika shule za msingi na sekondari zipewe kipaumbele kwenye bajeti hiyo.

Katibu wa CCM wa Wilaya ya Simanjiro Wambura Igembya amewapongeza madiwani hao kwa kupitisha rasimu ya mpango wa bajeti ya mwaka wa fedha wa 2026/2027.

Katibu wa Mbunge wa Jimbo la Simanjiro Dkt Frank Oleleshwa akitoa salamu za Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, James Ole Millya, amwelezea kwamba Bajeti ya 2026/2027 ilenge pia katika utatuzi wa migogoro ya ardhi.

Diwani wa Kata ya Loiborsiret, Ezekiel Lesenga Mardadi amesema anatarajia mwaka huu wa bajeti changamoto mbalimbali ikiwemo ukarabati wa barabara na vyumba vya madarasa na vitapatiwa ufumbuzi.

Diwani wa Kata ya Komolo, Saning'o Somi amesema mpango wa bajeti hiyo ni mzuri kwani utachangia maendeleo kwa wananchi wa eneo hilo.

CHAMA Cha Mapinduzi CCM kimesema kimeridhishwa na ujenzi wa mradi wa kituo cha kupooza umeme kilichopo Ziba wilayani Igunga mkoani Tabora.

Katibu wa NEC Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa CCM taifa Kenani Kihongosi alisema  hayo alipokagua ujenzi wa mradi huo uliogharibu shilingi bilioni 5.8 ambazo ni fedha za ndani kutoka Shirika la Umeme nchini TANESCO katika siku ya kwanza ya ziara yake ya siku tatu mkoani Tabora.

Mradi huo unahusisha ujenzi wa laini tano za matoleo ya umeme, ujenzi wa miundombinu ya umeme pamoja na ofisi ya kudhibiti mifumo ya vifaa vya umeme, ujenzi wa kibanda cha walinzi  ulinzi wa uzio wa kituo.

Awali Kihongosi alikagua mradi wa ujenzi wa shule ya Awali na Msingi Ibologero unaogharimu kiasi cha shilingi milioni 342.

Komredi Kihongosi alisifu jitihada za serikali za kuboresha sekta ya elimu kwa kujenga shule za viwango na madarasa ya kisasa akiwataka wananchi hao kuwapeleka watoto shule wakapate elimu.
















 


Upandaji wa miti ya asili ukiendelea kando kando ya mto Tighite katika kijiji cha Matongo

***

Katika mwendelezo wa utelekezaji wa mkakati endelevu wa kampuni ya Barrick, Mgodi wake wa North Mara uliopo wilayani Tarime mkoani Mara umefanikisha upandaji wa miti zaidi ya 40,000 kando ya mto Tighite kwa ushirikiano na shirika lisilo la kiserikali la Jamii wa Watumiaji wa Maji Tigithe Chini (JWMTC) kwa ajili ya kuhifadhi mazingira na kurejesha na uoto wa asili.

Mto Tighite ni moja ya vyanzo vikuu vya maji vya Mto Mara ambao unatiririsha maji yake katika Ziwa Victoria upande wa Tanzania na maelfu ya wakazi wa vijiji vilivyopo jirani na mgodi wa Barrick North Mara wanategemea mto huo kupata maji ya matumizi ya nyumbani, kunywesha mifugo na shughuli za kilimo.

Akiongea kuhusu programu hiyo ambayo inaendelea kupata mafanikio, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Watumia Maji Tigithe Chini (JWMTC), Mwita Seri, ameeleza kuwa kutokana na uwezeshaji na ushirikiano wanaoupata kutoka mgodi wa dhahabu wa Barrick North Mara hadi kufikia sasa wamefanikiwa kupanda miche ya miti 42,700.

“Tangu progamu hii ya kupanda miti kando ya mto Tighite izinduliwe mwaka jana wakati wa maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani tumekuwa tukipata ushirikiano mkubwa kutoka Mgodi wa North Mara na lengo lililokusudiwa la kutunza mazingira katika eneo hili linaendelea kupata mafanikio na eneo hili la mto limebadilika kwa kiasi kikubwa sasa”, amesema Mwita Seri.

Meneja Mkuu wa Mgodi wa Barrick North Mara, Apolinary Lyambiko amesema wakati wa uzinduzi wa progamu hiyo kuwa kuwa Dhamira ya mgodi ni kupanda miti ya asili 50,000 katika kingo za mto Tighite ili kuzuia mmomonyoko wa udongo kwa kushikilia udongo kwa mizizi yake ikiwemo na miti ya mbao itakayopandwa mita 60 za mto huo." Programu kama hizi ziliwahi kufanyika mto Mara . Dhumuni letu ndani ya mwaka mmoja tuwe tumekamilisha Programu hii" ,amesisitiza.

Wafanyakazi wa Mgodi wa Dhahabu wa Barrick North Mara wakishirikiana na wananchi kupanda miti ya asili kando kando ya mto Tighite wakati wa uzinduzi wa programu hiyo mwaka 2025.


Kwa mujibu wa Seri, uharibifu mkubwa wa uoto wa asili wa mto Tighite ndio uliisukuma taasisi ya Jumuiya ya Watumia Maji Tigithe Chini (JWMTC), kubuni wazo la kuwa na mpango endelevu wa kuhifandi mazingira ya chanzo hicho cha maji.


Amesema mgodi wa Barrick North Mara unagharimia ununuzi wa miche ya miti, uchimbaji mashimo na ulinzi wa miti iliyopandwa, miongoni mwa mambo mengine katika mradi huu.“Lengo kubwa ni kulinda mto Tighite kwa kurudisha uoto wa asili, na hata miti tunayopanda ni ya asili na rafiki kwa mazingira,” amesisitiza Mwenyekiti huyo wa JWMTC.


Seri amebainisha kuwa Jumuiya ya Watumia Maji Tighite Chini ambayo iko chini ya Bodi ya Maji Bonde la Ziwa Victoria, inasimamia kata nne zenye vijiji 12 jirani na mgodi wa Barrick North Mara. Alitaja vijiji hivyo na kata zake zikiwa kwenye mabano kuwa ni Matongo, Nyabichune, Nyangoto na Mjini Kati (Matongo), Nyamwaga na Komarera (Nyamwaga).


Vijiji vingine ni Nyakunguru, Nyarwana, Wegita na Keisaka (Kibasuka), Kewanja na Kerende (Kemambo).

Sehemu ya miche ya miti ya asili iliyooteshwa kwenye kitalu cha Jumuiya ya watumia maji Tighite Chini kwa ajili ya kupandwa kando kando ya mto Tighite

Mbali na kuwezesha utekelezaji wa mradi huu wa mazingira na kulinda chanzo cha maji cha mto Tighete Mgodi wa Barrick North Mara kupitia fedha za CSR umefanikisha mradi wa maji wenye thamani ya shilingi bilioni 2.665 kwa ajili ya upanuzi wa chanzo cha maji cha Nyamongo, wilayani Tarime vijijini kilichopo ndani ya eneo la Mgodi ambacho awali kilisanifiwa kuhudumia wananchi 27,742 wa vijiji vya Nyangoto, Matongo, Mjini Kati na Nyabichune na unasimamiwa na Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) na uko katika hatua za mwisho kukamilika.


Kutokana na ongezeko la mahitaji ya maji katika vijiji vingine saba vinavyozunguka mgodi. Chanzo hiki kimesanifiwa upya kwa lengo la kuhudumia wananchi 125,566 katika vijiji vingine sita vya Genkuru, Nyamwaga, nyakunguru, Kerende, Msege na Komarera.


Mgodi wa Dhahabu wa Barrick North Mara unaendeshwa na Kampuni ya Barrick kwa ubia na Serikali ya Tanzania kupitia Kampuni ya Twiga Minerals.


Kampuni ya Barrick kupitia utekelezaji wake wa mkakati endelevu inaendelea kufanikisha miradi mbalimbali ya kijamii katika maeneo yanayozunguka migodi yake hususani katika kuboresha sekta ya elimu, upatikanaji wa maji salama, afya, mazingira na kuongea wigo kwa ajira.



Wafanyakazi wa Taifa Gas na wadau wengine wakiwa na furaha katika moja ya vituo karibu na kilele cha Mlima Kilimxanjaro kwenye zoezi la kupanda mlima baada ya kampuni hiyo kudhamini programu ya kutangaza vivutio vya utalii na uhifadhi wa mazingira ambayo inaitwa “Guardians of the Peak” na kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia.

Kampuni ya Kusambaza Nishati ya nishati safi ya kupikia ya Taifa Gas , mwaka huu 2026 imeweka historia kubwa kwa kuwa mdhamini mkuu wa programu kutangaza vivutio vya utalii na uhifadhi wa mazingira ijulikanayo kama 'Guardians of the Peak' ambayo ilikuwa na kauli mbiu “Embrace Clean Energy, Protect Tomorrow” na kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia kwa ajili ya kulinda mazingira.


Programu hiyo pia ilihusisha upandaji wa miti na kupanda mlima Kilimanjaro ambapo wadau mbalimbali walishiriki wakiwemo baadhi yaa wafanyakazi wa Taifa Gas ambao walihakikisha Chapa ya kampuni inafika kileleni mwa mlima kuashiria mafanikio ya safari ya uthubutu, mshikamano na dhamira thabiti ya kufikia malengo makubwa.


Tukio hilo linaweka alama ya historia katika juhudi za kuiinua chapa ya Taifa Gas katika viwango vya juu zaidi, kwa nguvu, umoja na kujituma kwa timu nzima ya wafanyakazi wa kampuni.

Mtungi wa Taifa Gas kuelekea kileleni mwa Mlima Kilimanjaro

Timu ya Wafanyakazi wa Taifa Gas ikiwa katika hatua za safari ya kupanda kuelekea kileleni mwa Mlima Kilimanjaro, safari iliyojaa maandalizi, mshikamano na dhamira ya kupeperusha bendera ya kampuni katika paa la Afrika. Kupanda huku ni ishara ya uthubutu na ari ya kuendelea kufikia malengo makubwa





MERIDIANBET imepandisha kiwango kwa kushirikiana rasmi na Ruby Play, jina linalokuja kwa kasi kwenye ulimwengu wa sloti za mtandaoni. Ruby Play inaleta ubunifu, michoro ya kisasa na uzoefu wa kipekee wa uchezaji. Huu ni mwanzo wa historia mpya ya kasino mtandaoni, ambapo teknolojia ya hali ya juu inakutana na nafasi halisi za ushindi mkubwa.

Kwa Ruby Play, kila mchezo umeundwa kutoa uzoefu wa kipekee unaovutia kuanzia sekunde ya kwanza. Mandhari zake za kisasa, sauti zenye ubora na picha zenye mvuto huweka mchezaji katikati ya tukio. Ubunifu wao unaonekana wazi kupitia michezo yenye mwendo laini na vipengele vinavyoongeza msisimko kila unapozungusha. Hapa si tu kucheza, ni kuingia kwenye ulimwengu wa fursa, changamoto na nafasi halisi za kushinda.

Unaletewa mkusanyiko mpana wa michezo inayokidhi kila ladha ya mchezaji. Michezo kama Immortal Empress, Piggy Gold, Wild Thirst, Macau Beauties, na Bamboo Fortune zinathibitisha ubunifu wa Ruby Play katika kuchanganya utamaduni, ustadi na burudani ya kweli.

Meridianbet haikuachi nyuma, kuna michezo mbalimbali ya kasino mtandaoni pamoja na mechi za kimataifa za kubashiri zenye odds bomba zinazokuongezea nafasi ya kuongeza kipato chako kila siku. Kujiunga ni rahisi, Tembelea meridianbet.co.tz au piga *149*10#.

Kinachovutia zaidi ni namna Ruby Play inavyounda mbinu za ushindi zenye ubunifu wa hali ya juu. Wachezaji wana nafasi kubwa zaidi ya kubeba ushindi kutokana na vipengele maalum vilivyowekwa ili kuongeza msisimko na matarajio katika kila mzunguko. Kila mchezo ni tukio jipya, kila dakika ni fursa mpya, na kila ushindi ni motisha ya kuendelea kucheza.

Meridianbet sasa inakukaribisha kuingia kwenye hatua hii mpya ya kasino mtandaoni. Jiunge kupitia tovuti au application ya simu, ingia sehemu ya kasino na uchague michezo ya Ruby Play. Ulimwengu wa burudani ya kisasa na ushindi mkubwa umewasili, ni muda wako kung’aa.

Na Nasra Ismail, Geita

Wananchi wa Mitaa ya Magogo Ibolelo na 14 Kambarage, Kata ya Buhalahala, Manispaa ya Geita, wamemuomba Mbunge wa Jimbo la Geita Mjini, Chacha Wambura, kuwasaidia kufanya ukarabati wa barabara ambazo kwa sasa zimeharibika kwa kiasi kikubwa kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha.

Kutokana na mvua hizo, baadhi ya barabara zimekatika na nyingine kujaa maji, hali inayosababisha adha kubwa kwa watumiaji wa vyombo vya usafiri na wananchi kwa ujumla.

Kufuatia kilio hicho, Mbunge wa Jimbo la Geita Mjini, Chacha Wambura, ametembelea maeneo hayo kwa lengo la kujionea hali halisi ya ubovu wa miundombinu hiyo.

Wananchi wametumia fursa hiyo kueleza changamoto wanazokumbana nazo kila siku, zikiwemo kushindwa kufanya shughuli zao za kiuchumi na kijamii kutokana na ubovu wa barabara hizo, huku wakimuomba mbunge kuchukua hatua za haraka kunusuru hali hiyo.

Kwa upande wake, Mbunge wa Jimbo la Geita Mjini, Chacha Wambura, amewatoa hofu wananchi kwa kueleza kuwa tayari hatua stahiki zimeanza kuchukuliwa ili kukabiliana na changamoto zilizolalamikiwa.

Amesema kupitia ushirikiano wa ofisi yake, Ofisi ya Diwani na Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA), mipango ya matengenezo ya muda na ya kudumu inaendelea.

Wananchi wameonesha matumaini yao kuwa ahadi hiyo itatekelezwa kwa wakati ili kumaliza tatizo hilo ambalo limekuwa likiwakabili kwa muda mrefu.





 


Top News