WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, leo Mei 10, 2026 ameondoka nchini kuelekea Nairobi, Kenya ambako anatarajia kumuwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika Mkutano wa Ushirikiano wa Afrika na Ufaransa (Africa Forward: Africa–France Partnership for Innovation and Growth Summit) utakaofanyika Mei 11–12, 2026.

Lengo la mkutano huo ni kuendelea kuimarisha ushirikiano kati ya Afrika na Ufaransa katika sekta mbalimbali ikiwemo biashara, teknolojia, nishati, afya, Akili Unde (AI), kilimo, uchumi wa buluu pamoja na viwanda.

Aidha, mkutano huo unalenga kukuza uwekezaji mpya kati ya Afrika na kampuni za Ufaransa, kujenga ushirikiano unaotajwa kuwa wa usawa, pamoja na kujadili mageuzi ya mfumo wa fedha na maendeleo endelevu ya Afrika.

Mkutano huo wa Wakuu wa Nchi na Serikali unawakutanisha wadau wa maendeleo, wawekezaji pamoja na sekta binafsi, na umeandaliwa kwa ushirikiano kati ya Rais wa Jamhuri ya Kenya, Mheshimiwa William Samoei Ruto, na Rais wa Jamhuri ya Ufaransa, Mheshimiwa Emmanuel Macron.





Na Pamela Mollel,Arusha 

Jiji la Arusha linaendelea kushuhudia utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo inayolenga kuboresha huduma za kijamii pamoja na kuimarisha miundombinu katika maeneo tofauti ya jiji hilo. 

Hatua hiyo inaelezwa kuwa sehemu ya mkakati wa kuhakikisha Arusha linaendelea kuwa moja ya majiji muhimu nchini katika sekta ya utalii na shughuli za kikanda.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini humo, Meya wa Jiji la Arusha, Maxmillian Iranqhe, amesema katika kipindi cha robo ya tatu hadi mwisho wa mwaka wa fedha 2025/2026, halmashauri imeendelea kutekeleza miradi yenye thamani ya mabilioni ya shilingi katika kata mbalimbali kwa lengo la kuleta maendeleo kwa wananchi.

Miongoni mwa miradi inayoendelea ni ujenzi wa Kituo cha Polisi katika Kata ya Moshono unaogharimu zaidi ya shilingi milioni 145. Pia kuna ujenzi wa mtaro wa Suye wenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 100, mradi unaotarajiwa kusaidia kupunguza changamoto za miundombinu ya maji ya mvua katika eneo hilo.

Katika kuboresha mazingira na usimamizi wa taka, Halmashauri ya Jiji la Arusha inaendelea na ujenzi wa vifuko viwili vya kuhifadhi taka katika Kata ya Muriet kwa gharama inayozidi shilingi milioni 64.

 Sambamba na hilo, magari mawili mapya aina ya Toyota Pick Up yenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 363 yamepokelewa ili kusaidia shughuli za utoaji wa huduma za kijamii.

Sekta ya elimu nayo imeendelea kupewa kipaumbele ambapo ujenzi wa Shule ya Sekondari Bondeni City unaendelea kwa gharama ya zaidi ya shilingi milioni 760.

Aidha, ujenzi wa Shule ya Msingi Ungalimited nao unaendelea kwa zaidi ya shilingi milioni 877 ikiwa ni jitihada za kuongeza mazingira bora ya kujifunzia kwa wanafunzi.

Meya Iranqhe amesema utekelezaji wa miradi hiyo unaonesha dhamira ya halmashauri katika kuimarisha maendeleo ya jiji pamoja na kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora zinazokidhi mahitaji yao ya kila siku.

Aidha, amewataka wananchi kuendelea kushirikiana na halmashauri katika kulinda na kuthamini miradi hiyo ili iweze kuleta manufaa ya muda mrefu kwa jamii na kuchochea maendeleo endelevu ya Jiji la Arusha.



Na  Byera Deus,Kagera 

SERIKALI kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kushirikiana na Benki ya Maendeleo ya kilimo(TADB) imeendelea na utoaji wa mikopo isiyo na riba na yenye masharti nafuu kwa ajili ya utekelezaji  wa miradi ya ufugaji wa samaki kwenye vizimba ili kuwezesha vijana wengi kujiajili kupitia uvuvi.

Akizungumza katika  halfa ya uzinduzi wa kukabidhi mitaji ya kuwezesha utekelezaji wa miradi iliyobuniwa  na Vijana wa (Build Better Tomorrow (BBT)-Uvuvi Mkoa wa Kagera katika mwalo wa -Bilolo Kemondo  Mwakilishi wa Katibu Mkuu Wizara hiyo Emelda Adam amesema programu hiyo inalenga kupambana na changamoto ya ajira kwa vijana na kuongeza nguvu ya vijana kujitegemea 

Amesema vijana walionufaika na vizimba mkoani Kagera walipata mafunzo ya ukuzaji wa viumbe hai mwaka 2024  na wametoka mikoa mbalimbali wakiwa wameiva kwa ujuzi wa uendeaji wa vizimba hivyo ambapo wataanza kuvuna Samaki baada ya miezi 7.

Kwa upande wake Msimamizi Mkuu wa programu ya “BBT” Kanda ya Ziwa Peter Masumbuko amesema vijana 47 wa Mkoa wa Kagera wamenufaika na programu hiyo.Shilingi bilioni saba zimetengwa kwa ajili ya vijana  zaidi ya 300 wa mikoa ya kanda ya ziwa.

Ameongeza kwa Kanda ya ziwa Program ya kuwanuia vijana mpaka kujiajiri inatekezwa mikoa ya Kagera,Mwanza ,Geita na Mara na vijana hao wote wameisha hitimu mafunzo yao

Amefafanua kwa kuanzia Kila kijana anapata kuzimba kimoja japo wanawaweka katika makundi na mradi unakuwa na  Nyumba ya mlinzi Boti ya ufatiliaji na Camera ya Kuona Nini kinaendelea katika mradi huo ambao serikali itawalea vijana kwa miaka minne Hadi wajikimu

Awali Mkuu wa Wilaya Erasto Sima kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Kagera Ramadhan  Kido amesema  ametumia nafasi hiyo kumshukuru Rais Dk.Samia Suluhu Hassan kwa ajili ya programu hiyo na kuwaasa vijana wanufaika wa mkopo huo kuutumia kwa malengo yaliyokusudiwa.

Amesema baada ya ufunguzi wa vizimba mvuvi yeyote atakayekamatwa katika  eneo hilo atachukuliwa kama mvuvi haramu kwani sehemu hiyo haipaswi kusogelewa badala yake inatakiwa kulindwa Kwa nguvu zote ili kuleta matokeo Chanya .

Wakati huo huo Mwenyekiti wa Halmashauri ya Bukoba Sadothi Ijunga ameishukuru Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kuukumbuka mkoa wa Kagera huku akitoa rai kwa vijana kuwa na nidhamu katika matumizi ya fedha walizozipata.

Katika hatua nyingine baadhi ya wanafuika akiwemo Marius Pius amesema  mafunzo waliyopatiwa yamehusisha vijana wa aina zote na wanamshukuru Rais Dk.Samia kwa kutimiza ahadi yake kwa vijana hao.

“Tulikuwa tayari tuko mtaani baada ya mafunzo lakini leo jambo limetimia ,hivyo sisi kama vijana lazima tusimame imara na tulete matokea chanya ambayo pia yatasaidia vijana wengine  kujiajili.Tuko tayari kulinda vizimba hivi na kuzalisha kwa weledi,”amesema Pius.












Na Said Mwishehe,Michuzi TV

SERIKALI ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dk.Samia Suluhu Hassan imeendelea kujenga mahusiano mema na nchi jirani zikiwemo za Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Mahusiano hayo ya Tanzania na nchi jirani yamekuwa ya kihistoria na chini ya uongozi wa Rais Dk.Samia umeweka msingi imara wa kuendeleza ujirani huo hasa ujirani wenye tija kwa nchi hizo.

Ujirani wetu kati ya Tanzania na nchi za jumuiya hiyo umewezesha Mei 3,2026 kushuhudia ujio wa Rais wa Rwanda Paul Kagame na Mei 4 Rais wa Jamhuri ya Kenya Dk.William Ruto .Ni safari za marais wawili tofauti lakini msingi wa safari yao ni muelekeo ule ule wa kujenga uhusiano na ujirani mwema kwa nchi hizo.

Hata hivyo ujio wa Rais Kagame na Rais Rutto pia ni uthibitisho wa nafasi ya Tanzania ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki

Kwa kukumbusha tu nafasi ya Tanzania ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) ni pana na ya kimkakati, ikihusisha historia, uchumi, siasa, na usalama wa kikanda. Hapa chini kuna maelezo ya kina yanayokupa picha kamili:

Iko hivi katika historia ya jumuiya hiyo inaonesha Tanzania ni mwanachama mwanzilishi wa EAC (toleo la sasa lililoanzishwa mwaka 2000), pamoja na Kenya na Uganda. Pia ilishiriki katika Jumuiya ya zamani ya Afrika Mashariki iliyovunjika mwaka 1977.

Tanzania imekuwa nguzo ya mshikamano wa kikanda, ikisisitiza ushirikiano wa polepole lakini thabiti (“gradual integration”).Uwepo wa Tanzania umechangia katika kuweka misingi ya sera na taasisi za EAC.

Kwa upande wa kiuchumi Tanzania ina mchango mkubwa katika uchumi wa EAC hasa katika Bandari na Biashara.Katika Bandari ya Dar es Salaam ni lango muhimu kwa biashara ya nchi zisizo na bandari kama Rwanda, Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

Pia Tanzania inaunganisha ukanda wa EAC na masoko ya kimataifa kupitia Miundombinu Reli, barabara, na miradi ya nishati husaidia kuunganisha nchi wanachama.

Mfano ni miradi ya reli ya kisasa (SGR) inayolenga kuboresha usafirishaji.Miradi mingine ni Soko la Pamoja ambapo Tanzania ni sehemu ya Soko la Pamoja la EAC (Common Market) – kuruhusu uhuru wa watu, ajira, huduma na mitaji.

Mara nyingi Tanzania imekuwa makini zaidi katika kufungua soko lake kikamilifu ikilinganishwa na baadhi ya wanachama.

Kwa upande wa nafasi ya kisiasa na kidiplomasia Tanzania ina mchango mkubwa katika diplomasia ya kikanda na inajulikana kwa sera ya kutafuta maelewano na amani.Jambo kubwa na la kufurahisha zaidi Tanzania mara nyingi husimama kama mpatanishi muhimu.


Hivyo kwa ujumla, Tanzania ni mhimili wa utulivu, uchumi, na sera za tahadhari ndani ya EAC. Inachangia kwa kiasi kikubwa katika maendeleo ya jumuiya, huku ikihakikisha maslahi yake ya kitaifa hayapotei katika mchakato wa ujumuishaji wa kikanda.

Nimeeleza kwa kifupi kuhusu nafasi ya Tanzania katika jumuiya hiyo na ujio wa Rais Kagame na Rais Dk.Ruto inaendelea kuthibitisha nafasi na mchango wake kwa nchi hizo.

Hata moja ya mambo ya kuvutia kwa Rais Dk.Samia Suluhu Hassan ni kuona anaendelea kuwa daraja la mahuasiano mema kati yake na nchi jirani. Ile falsafa yake ya 4R imepenya hata katika nchi zinazoizunguka Tanzania.Hizi R4 za Mama zimepenya na kuwa nguzo ya diplomasia, amani na umoja wa Afrika Mashariki

Ikumbukwe katika kipindi cha hivi karibuni, ukanda wa Afrika Mashariki umeshuhudia mijadala mbalimbali ya kisiasa na kijamii iliyovuka mipaka ya nchi moja kwenda nyingine. 

Katika mazingira hayo, falsafa ya “R4 za Mama” imeendelea kujidhihirisha kama dira muhimu ya diplomasia, utulivu na ujenzi wa mahusiano yenye tija kwa taifa na ukanda mzima.

Kwa mtazamo wa wengi, R4 zimeonyesha msimamo wa kulinda heshima, mamlaka na uhuru wa Tanzania bila kuingia katika mvutano usio wa lazima sio tu nchini bali na kwa nchi nyingine za jumuiya ya Afrika Mashariki.

Hii ni kwa sababu taifa lolote huru lina haki ya kuendesha masuala yake ya ndani kwa mujibu wa sheria, taratibu na utashi wa wananchi wake. 

Kauli au matendo yanayoonekana kuingilia uhuru wa nchi nyingine mara nyingi huweza kuathiri mshikamano wa kikanda na kuzua taharuki zisizo za lazima.Ndio maana Rais Dk.Samia anaamini katika maridhiano zaidi .

Hata hivyo, nguvu kubwa ya R4 haipo tu katika kujibu changamoto za kisiasa, bali katika uwezo wake wa kujenga madaraja ya ushirikiano na ujirani mwema. 

Tanzania imeendelea kuonesha diplomasia ya kisasa siyo ya migogoro na majibizano, bali ni ya hekima, mazungumzo na mshikamano wa kikanda. Huo ndio msingi unaoifanya Afrika Mashariki kuendelea kuwa eneo lenye matumaini makubwa ya maendeleo ya pamoja.

Ukanda wa Afrika Mashariki una historia, tamaduni na udugu unaowaunganisha wananchi wake. Mataifa haya yanategemeana katika biashara, uwekezaji, usafirishaji, utalii na hata masuala ya usalama. 

Kwa sababu hiyo, kauli za uchochezi au matusi hazina nafasi katika kujenga mustakabali wa pamoja. Kinachohitajika ni kuheshimiana, kusikilizana na kushirikiana kwa maslahi ya wananchi wa ukanda huu.

Ujio wa Rais Kagame na Rais Rutto ni uthibitisho wa kwamba R4 zimeendelea kuonesha umuhimu wa kudumisha amani na usalama kama msingi wa maendeleo ya kiuchumi. 

Hakuna uchumi imara bila utulivu wa kisiasa, na hakuna ushirikiano wa kweli bila kuheshimu mipaka na mamlaka ya kila taifa. Tanzania, kupitia misingi hiyo, imeendelea kuwa mfano wa nchi inayotanguliza maridhiano, diplomasia na ushirikiano wa kimataifa.

Kwa ujumla, falsafa ya R4 za Mama siyo tu kauli ya kisiasa, bali ni mwelekeo unaolenga kujenga Afrika Mashariki yenye mshikamano, heshima ya mataifa, maendeleo ya pamoja na amani ya kudumu. 

Katika dunia ya leo yenye changamoto nyingi za kisiasa na kiuchumi, diplomasia ya hekima ndiyo silaha muhimu zaidi kuliko mabishano ya mitandaoni au siasa za mgawanyiko.

Wakiwa nchini Tanzania Rais Kagame na Rais Dk.Rutto kila mmoja kwa nafasi yake wamepata nafasi ya kuzungumza na mwenyeji wao Rais Dk.Samia Suluhu Hassan.

Akizungumza mazungumzo yake na Rais Kagame, Rais Dk. Samia alisema Tanzania na Rwanda  zimeendelea kujenga uhusiano wa undugu, ujirani mwema na wa kihistoria, unaoakisi  mshikamano wa muda mrefu kati ya wananchi wa pande zote.

Dk. Samia pia alisema  biashara kati ya Tanzania na Rwanda imeendelea kukua na kufikia thamani ya sh. bilioni 644 mwaka 2025 na kuanzia mwaka 1990 hadi Machi, 2026, Mamlaka ya Uwekezaji Tanzania imesajili miradi 42 ya uwekezaji kutoka Rwanda yenye thamani ya dola za Marekani milioni 325.5, iliyozalisha ajira 2,225 kwa Watanzania.

Pamoja na hatua hiyo, Rais Dk. Samia alisema nchi zote zimekubaliana kuongeza kasi ya kuondoa changamoto za kibiashara, vikiwemo vikwazo visivyo vya kikodi, kupanua biashara na uwekezaji, na kutumia kikamilifu fursa za soko la pamoja la Afrika Mashariki na Soko Huru la Biashara la Afrika.

Kama ilivyokuwa kwa Kagame, ziara ya Rais Dk.Ruto pia imebeba matumaini ya kuimarisha ushirikiano wa kindugu na kimkakati kati ya Tanzania na Kenya katika biashara, uwekezaji, miundombinu, usafirishaji na maeneo mengine ya maslahi ya pamoja.

Ukweli wa mambo ni kwamba Rais Dk. Samia Suluhu Hassan anastahili pongezi kwa kutekeleza kwa vitendo ahadi ya kujenga diplomasia ya uchumi,siasa na kijamii ambayo mwanzoni kabisa baada ya kuapishwa kushika uongozi wa nchi aliahidi kusimamia na kufanikisha hilo.

Ni wakati wa Watanzania wote kila mmoja kwa nafasi yake kutambua jitihada za Rais Dk.Samia za kuendelea kujenga mahusiano ambayo yanakwenda kufungua fursa mbambali za biashara.

Tunakumbuka wakati Rais Dk.Ruto pamoja na kuelezea masuala mbalimbali yanayohusu nchi hizo hakusita pia Kenya na Tanzania sio tu majirani bali ni ndugu wa kweli ambapo alitoa mifano kadhaa kuthibitisha anachokisema baina ya nchi hizo.

Hata hivyo nimalizie kwa kueleza hivi Tanzania chini ya uongozi mahiri wa Rais Samia iko katika mikono salama na kauli mbiu ya Kazi na Utu tunasonga mbele imekuwa faraja kwa kila mkoja wetu.


Kwa maoni 0713833822/0762451570


Na Mwandishi Wetu

KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imesema kuwa uwekezaji unaofanywa na Oryx Energies Tanzania Limited ni kielelezo cha mafanikio ya juhudi za Serikali katika kuimarisha sekta binafsi na kuongeza mchango wake katika maendeleo ya taifa.

Hayo yameelezwa leo Mei 9,2026 jijini Dar es Salaam wakati Kamati hiyo ilipotembelea sehemu maalumu ya uzalishaji wa bidhaa za Kampuni ya Oryx Energies Tanzania Limited.

Akizungumza katika ziara hiyo, Mwenyekiti wa kamati hiyo Subira Mgalu amesema kamati hiyo inatambua mchango na uwekezaji uliofanywa na Oryx Energies ambapo katika kipindi cha miaka minne imechangia pato la taita Sh.trilioni 1.2  huku pia ikiwa imetoa ajira za moja kwa moja  1000 na kwa asilimia kubwa walioajiriwa ni vijana wa kitanzania.

“Katika uwepo wa miaka 25 ya Oryx Energies nchini imetoa mchango mkubwa katika kuwezesha Watanzania kupata ajira lakini pia imekuwa na mchango mkubwa katika kuleta maendeleo na kukuza uchumi wa Taifa la Tanzania.”

“Wabunge wamepata fursa ya kuona mambo mazuri kupitia kampuni hii ikiwemo  maabara ya kisasa kwa ajili ya kupima ubora wa vilainishi lakini kwa upande wa ajenda ya matumizi ya nishati safi ya kupikia majumbani hivi sasa kumekuwepo na ongezeko kubwa la watumiaji kutoka asilimia  sita ya awali hadi kufikia asilimia 26 na ongezeko hili linakchango mkubwa wa Oryx Gas na wadau wengine.”

Aidha katika nishati safi ya kupikia amesema kamati ya nishati inampongeza Rais Dk.Samia Suluhu Hassan kwani ndio kinara wa nishati safi na amekuwa akihamasisha matumizi ya nishati hiyo na sasa anatambulika katika medani za kimataifa.

Pia Mgalu amesema kamati hiyo inaendelea kusisitiza uwekezaji wenye tija na unaoleta matokeo katika taifa letu  lakini kubwa mchango wa kuinua uchumi wa nchi na watanzania kwa ujumla wake.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Oryx Energies Tanzania Limited Imani Mtafya amesema kampuni hiyo imekuwepo kwa miaka 25 sasa na uwepo wake umetoa mchango mkubwa kwa Watanzania na hasa kuhakikisha wanapata bidhaa bora hasa ya vilainishi.

Aidha amesema Oryx Energies kwa mwaka inachangia Sh.bilioni 300 ambayo ni sawa na asilimia 0.1 sambamba na kuwa na ajira asilimia 99 kwa watanzania .

Wakati huo huo Mkurugenzi wa Oryx Gas Tanzania Benoite Araman amewahakikishia wabunge wa kamati hiyo kuwa kampuni hiyo itaendelea kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini ikiwa ni sehemu ya juhudi zao katika kuiunga mkono Serikali ambayo imelenga ifikapo mwaka 2030 asilimia 80 ya Watanzania iwe inatumia nishati safi ya kupikia.








Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Paul Makonda, amesema Serikali inaendelea kuweka mikakati  ya kuboresha elimu ya michezo, pamoja na kuinua uwezo wa walimu wa fani hiyo hapa nchini, ili kuhakikisha wanafunzi wanapata maarifa bora kwa maendeleo ya vipaji vyao.

Akizungumza  katika hafla ya usiku wa Tuzo kwa  Wanamichezo zilizoandaliwa na Baraza la Michezo la Taifa (BMT)  tarehe 9 Mei, 2026, Mhe.  Makonda amesema, kuna umuhimu wa kuendelea kuwajengea walimu uwezo kupitia programu maalum za mafunzo ili waendane na mahitaji ya sasa. 

Ameeleza kuwa, hatua hiyo itasaidia walimu kuelewa vizuri mbinu za ufundishaji pamoja na kuwasaidia wanafunzi kutambua vipaji vyao katika michezo  mapema.

"Serikali inalenga kuhakikisha walimu wanaopata nafasi ya kufundisha michezo  katika shule zetu wanakuwa na sifa na uelewa unaotakiwa ili kuongeza ubora wa elimu ya michezo.Tunaendelea kuboresha mazingira bora ya kazi, pamoja na motisha kwa walimu  zitakazowawezesha kufanya kazi kwa bidii" alisema Mhe. Makonda.

Ameongeza  kuwa, Serikali itaendelea kushirikiana na jamii pamoja na wadau mbalimbali ili kuhakikisha sekta ya michezo  inazidi kuimarika na kutoa wataalamu wenye ushindani na ubunifu.

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amechochea kufanyika  kwa mageuzi makubwa katika sekta ya michezo nchini.

Amesema hayo jana Jumamosi (Mei 9, 2026) alipomwakilisha Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi,  Mheshimiwa Dkt. Hussein Ali Mwinyi, katika hafla ya utoaji tuzo za michezo za Baraza la Michezo la Taifa  (NSCA), zilizofanyika kwenye ukumbi wa The Super Dom, Masaki jijini Dar es Salaam.

Mheshimiwa Dkt. Mwigulu amesema Mheshimiwa Rais Samia amefanya mambo mengi yanayodhihirisha nia yake ya dhati ya kuendeleza michezo nchini.

"Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amefanya mageuzi makubwa kwenye michezo, kuanzishwa kwa mfuko wa maendeleo ya michezo ni miongoni mwa mambo makubwa kwenye sekta ya michezo." Amesema Waziri Mkuu Mwigulu.

Waziri Mkuu ameongeza kwa kusema kuwa "Goli la mama na knock out ya mama vimeongeza ari kwa wanamichezo na vilabu vyetu vya Tanzania, kama mlivyoona timu zetu zimefanya vizuri kwenye mashindano ya kimataifa, hii ni kutokana na chachu iliyoletwa na goli la mama."

"Ninyi wenyewe ni mashuhuda, miaka ya nyuma timu zetu zilikuwa zikipangwa na timu za kaskazini na magharibi tulikuwa tunajua ni wasindikizaji tu, lakini kwa sasa, kibao kimegeuka, nchi yetu inafanya vizuri na inazungumzwa vizuri." Amesisitiza Dkt. Mwigulu.

Pamoja na hayo, Waziri Mkuu amesema eneo lingine linalodhihirisha kuwa serikali inaipa michezo kipaumbele ni uwekezaji katika miundombinu, mathalani ujenzi wa uwanja wa AFCON Arusha na ukarabati mkubwa wa uwanja wa Benjamin Mkapa.

"Haya yote yataendelea kuweka chachu ya mafanikio katika sekta ya michezo nchini. Nikiwa Msimamizi Mkuu wa shughuli za Serikali, nitaendelea kusimamia vizuri maono haya ya Rais wetu ili yatoe matokeo yaliyokusudiwa." Amesema Waziri Mkuu.

Akizungumzia tuzo hizo, Waziri Mkuu amesema ni motisha muhimu kwa wadau wa michezo nchini na  sehemu ya mkakati wa kuimarisha maendeleo ya michezo na jukwaa muhimu la kuwatambua wanamichezo wanaoliwakilisha vyema Taifa, ndani na nje ya nchi.

Kutokana na umuhimu wanamichezo kutambuliwa vipaji vyao kuanzia kwenye umri mdogo, Waziri Mkuu ameitaka Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kuhakikisha inalinda maeneo ya wazi yaliyotengwa kwa ajili ya michezo ili vijana wa Kitanzania wapate majukwaa ya kuonesha vipaji vyao.

Wadau mbalimbali wa michezo, wakiwemo wachezaji, wanahabari na viongozi wa michezo waliofanya vizuri kwa mwaka 2025 wametambuliwa na kupewa tuzo.









 

Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga, amewashauri Wamiliki wa Viwanda vipya Kutoa kipaumbele kwa wazawa katika ajira ili kukuza uchumi na mapato ya Taifa kwa ujumla.

Akizungumza wakati wa akifungua wa Kiwanda kipya cha kutengeneza tambi za papo hapo (Instant) cha Kura Food mkoani Pwani, amesema kuwa Serikali inaendelea kuboresha mazingira ya Biashara ikiwemo sera, miundombinu, na mifumo ili kuvutia Wawekezaji na wafanyabiashara na kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania kimataifa.

Aidha, Wizara imefanya mapitio ya sheria na kanuni ili kuhakikisha zinajielekeza katika kuwezesha biashara na kuondoa vikwazo badala ya kudhibiti pekee. Lengo ni kushirikiana na wadau wa mnyororo wa thamani, kutumia teknolojia za kisasa zinazoongeza tija, uzalishaji, na ufanisi wa biashara nchini.

Naye, Mwenyekiti wa Kura Food, Bw. Wu Yeping, ameipongeza Serikali kwa kuweka mazingira rafiki yanayorahisisha uwekezaji,

Huku Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Mhe. Abubakar Kunenge, akibainisha kuanza kwa uboreshaji wa miundombinu ya barabara na Reli ya Kisasa (SGR) kuanzia mwaka ujao ili kufungua zaidi fursa za kibiashara mkoani humo.

Naye Mbunge wa Kisarawe, Mhe. Selemani Jafo, amemshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa sera zake thabiti ambazo zimekuwa chachu ya kuvutia wawekezaji. Sera hizi zimesaidia kwa kiasi kikubwa kupunguza changamoto ya ukosefu wa ajira kwa wananchi wa jimbo hilo kupitia kuanzishwa kwa viwanda vipya.

            
Na Farida Mangube Morogoro.

Katika juhudi za kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi na uharibifu wa mazingira unaoendelea kuathiri jamii na rasilimali za asili, wadau wa sekta ya mazingira wamekutana mkoani Morogoro kujadili utekelezaji wa Mradi wa RESOLVE NbS (Suluhisho), unaolenga kutumia masuluhisho ya asili kurejesha mazingira yaliyoharibika na kuimarisha maisha ya wananchi.

Semina hiyo imewakutanisha wadau kutoka maeneo mbalimbali yanakotekelezwa mradi huo kwa lengo la kujenga uelewa wa pamoja kuhusu malengo, utekelezaji na matokeo yanayotarajiwa katika kipindi cha miaka mitatu ya mradi huo kuanzia mwaka 2025 hadi 2027.

Mradi wa RESOLVE NbS unatekelezwa kwa ushirikiano wa taasisi mbalimbali zikiwemo Shirikisho la Uhifadhi wa Mazingira Asilia Duniani (IUCN), WWF, CARE, EAMCEF, CAN na CEoT katika mikoa ya Morogoro na Iringa.

Akizungumza katika semina hiyo, Afisa Programu wa IUCN, Abdulaziz Mkwizu, alisema mradi huo umeanza kutekelezwa katika halmashauri tano ambazo ni Ifakara Mji, Mlimba, Morogoro Vijijini, Iringa Vijijini pamoja na Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo.

Alisema mradi huo utajikita katika kuboresha mipango ya matumizi bora ya ardhi, kurejesha ikolojia za misitu, ardhi na mito iliyoharibiwa pamoja na kuimarisha uwezo wa jamii kupitia vikundi vya kuweka na kukopa (VSLA).

“Mradi huu pia utasaidia jamii kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi kwa kuhamasisha kilimo mseto kinachozingatia bayonuai na kuboresha mifumo ya uzalishaji wa mazao kupitia vyama vya ushirika vya AMCOS,” alisema Mkwizu.

Kwa upande wake, Mratibu wa Mradi kutoka WWF, Josia Japhet Ngamagila, alisema lengo kuu la RESOLVE NbS ni kuhakikisha jamii pamoja na rasilimali za asili zinakuwa na uwezo mkubwa wa kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi kwa kutumia suluhisho zinazotokana na mazingira asilia.

Alisema mafanikio ya mradi huo yatategemea ushirikiano wa karibu kati ya wadau wote wanaoshiriki utekelezaji wake pamoja na ushirikishwaji wa jamii katika maeneo husika.

Ngamagila aliongeza kuwa semina hiyo imekuwa hatua muhimu ya kuwakutanisha wadau mbalimbali ili kuwa na maono ya pamoja katika utekelezaji wa mradi huo unaotarajiwa kuwa chachu ya uhifadhi wa mazingira na maendeleo endelevu kwa jamii za Morogoro na Iringa.

Baadhi ya washiriki wa semina hiyo walieleza kufurahishwa na elimu waliyoipata kuhusu utekelezaji wa Mradi wa RESOLVE NbS, wakisema utasaidia kuongeza uelewa wa jamii juu ya umuhimu wa uhifadhi wa mazingira na matumizi endelevu ya rasilimali za asili.

Walisema kupitia mafunzo hayo wamepata mwanga kuhusu namna bora ya kushiriki katika shughuli za uhifadhi, kilimo kinachozingatia mazingira pamoja na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi katika maeneo yao.

Aidha walitaka kuwepo kwa ushirikishwaji mkubwa wa wananchi katika hatua zote za utekelezaji wa mradi huo ili kuhakikisha manufaa yake yanaifikia jamii moja kwa moja pamoja na kuleta matokeo chanya katika uhifadhi wa mazingira na maendeleo ya kijamii.










Top News