Na Mwandishi Wetu, Tabora

NAIBU Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Bara,John Mongella, kwa niaba ya Katibu Mkuu wa CCM, Balozi Dkt. Asha-Rose Migiro, ameshiriki katika ibada ya mazishi ya aliyekuwa Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM ya Taifa mstaafu, Ndugu Nassor Hamdani.

Mazishi hayo yamefanyika leo Februari  3,2026 katika makaburi ya Mihogoni, Kata ya Mbugani, Manispaa ya Tabora mkoani Tabora. 

Akizungumza katika ibada hiyo,Mongella amewasilisha salamu za rambirambi kutoka Chama Cha Mapinduzi, akimuelezea marehemu ndugu Nassor Hamdani kuwa alikuwa mshauri mwema wa Chama kwa kipindi chote cha uhai wake, sambamba na mchango wake mkubwa wa kujitolea kwa jamii.

Amesema CCM itaendelea kumkumbuka marehemu kwa uadilifu, hekima na mchango wake katika kukijenga Chama pamoja na ustawi wa jamii kwa ujumla.












 

Na FARIDA MANGUBE, MOROGORO

Baada ya mafuriko makubwa ya mwaka 2024 kukata mawasiliano na kuhatarisha maisha ya wananchi wa Kata ya Ngerengere, hali iliyosababisha adha kubwa ya usafiri na kudhoofisha shughuli za kiuchumi, Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kupitia wakala wa barabara mijini na vijijini TARURA mkoa wa Morogoro ililazimika kuchukua hatua za haraka kutatua changamoto hiyo ya muda mrefu.

Serikali ilitenga jumla ya shilingi 200,000,000 kwa ajili ya ujenzi wa daraja la upinde wa mawe katika barabara ya Ngerengere – Sinyaulime lenye  urefu wa mita 30 na midomo miwili ya kupitisha maji, sambamba na uchongaji wa barabara yenye urefu wa kilometa moja, mradi uliolenga kurejesha mawasiliano ya uhakika na usalama wa usafiri kwa wananchi wa eneo hilo.

Akizungumza na Michuzi Blog kwenye ziara ya kamati ya siasa Mkoa wa Morogoro iliyokuwa ikikagua miradi ya barabra ndani ya Halmashauri hiyo Mwenyekiti wa Kijiji cha Sinyaulime Shabani Ramadhani  amesema kwa muda mrefu walikuwa wakikabiliwa na adha ya usafiri na usafirishaji, hususani nyakati za mvua, baada ya daraja hilo kusombwa na maji  na kukatiza mawasiliano, kuhatarisha maisha ya wananchi na kudhoofisha shughuli za kiuchumi.

Kwa mujibu wa taarifa ya utekelezaji iliyowasilishwa kwa Kamati ya Siasa ya CCM Mkoa wa Morogoro katika maadhimisho ya miaka 49 ya kuzaliwa kwa chama hicho, mkandarasi M/S Yesaca Civil and Building Works Company Limited anaendelea na kazi bila kuwasilisha madai ya malipo hadi sasa, huku thamani ya mradi ikifikia shilingi 199,668,112.

Mradi huo wa dharura unasimamiwa na TARURA Wilaya ya Morogoro hadi sasa, utekelezaji wa mradi huo umefikia asilimia 80, huku unatarajiwa kukamilika Aprili 8, 2026, baada ya ratiba ya awali kuathiriwa na changamoto za mvua.

Kazi zinazoendelea ni pamoja na ujenzi wa kuta za daraja, uchongaji wa barabara, uwekaji wa kifusi, ujenzi wa kinga za daraja (gabions), uwekaji wa guard rail pamoja na kuvunja daraja la zamani, hatua zinazolenga kuhakikisha daraja linakuwa imara, salama na la kudumu.

Aidha baada ya kutembela na kukagua  kamati ya Siasa ya CCM Mkoa wa Morogoro imelidhika na utekelezaji wa mradi huo na kuipongeza TARURA kwa usimamizi mzuri, ikisisitiza kuwa barabara ni kiungo muhimu katika kukuza uchumi na ustawi wa jamii.

Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Morogoro, Mhandisi Joseph Masunga, amesema kukamilika kwa daraja hilo kutarahisisha huduma za usafiri na usafirishaji kwa wakazi wa maeneo hayo, hususani katika kusafirisha mazao ya kilimo na kufikia masoko ya ndani na nje ya nchi.

Kwa upande wake, Meneja wa TARURA Mkoa wa Morogoro Mhandisi Emmanuel Ndyamukama amesema wakala huo umejipanga kuhakikisha maeneo yote korofi nyakati za mvua yanaboreshwa ili kurahisisha huduma kwa wananchi, kulingana na Ilani ya Chama Cha Mapinduzi.

Nae Katibu wa CCM mkoa wa Morogoro Nuru Ngereja ameitaka TARURA na TANROADS kukamilisha miradi yote inakamika kwa wakati ili kukidhi hitaji la watanzania huku ikisisitiza kutoa kazi kwa wakandalasi wanaotekeleza miradi kwa wakati.

Wadau wa maendeleo wameeleza kuwa ujenzi wa daraja hilo ni ushahidi wa utekelezaji wa ahadi za Serikali ya Awamu ya Sita na Ilani ya CCM kwa vitendo, hasa katika kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi na kuimarisha miundombinu ya vijijini.



 

Tume ya Ushindani (FCC) imeweka mikakati mbalimbali ya kuimarisha utoaji wa huduma bora kwa wananchi kwa wakati, kupitia matumizi ya mifumo ya kisasa katika utekelezaji wa majukumu yake.

Akizungumza wakati wa kikao kazi na watumishi wa Tume hiyo kwa lengo la kupanga mikakati ya utekelezaji wa majukumu, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, Bi. Khadija Ngasongwa, amesema hatua hizo zinalenga kuongeza ufanisi wa huduma na kuwahudumia wananchi kwa viwango vya juu vya ubora.

Amesema FCC inaendelea kutekeleza dhamira ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ya kuhakikisha mazingira ya biashara nchini yanaboreshwa na kuwashirikisha wafanyabiashara kupitia mifumo rafiki na yenye ufanisi.

Ngasongwa amesema kuwa katika kipindi cha siku 100 za uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, FCC imekuwa ikichukua hatua mbalimbali za kusogeza huduma karibu na wananchi, ikiwemo kuanzisha Ofisi ya FCC Mkoa wa Tanga na Mipakani ili kuongeza wigo wa utoaji huduma na kuwafikia wananchi wengi zaidi, hususan wale waliopo maeneo ya pembezoni mwa nchi. 

Ameongeza kuwa FCC imeendelea kudumisha cheti hicho cha ubora kutokana na jitihada zake katika utoaji wa huduma kwa wananchi na wadau wa biashara kwa weledi na uwazi.

“Tuko hapa kwa ajili ya kutoa huduma kwa wananchi kwa viwango vya ubora vinavyotambulika kimataifa, niwapongeze kwa kuendelea kushikilia Cheti cha Ithibati ya Ubora ISO 9001:2015,” amesema Ngasongwa.

Vilevile watumishi walipata nafasi ya kupitishwa na kujadili tathmini ya rasimu ya Mpango Mkakati Mpya wa Tume wa miaka mitano (Strategic Plan) 2026/27-2030/31 unaoakisi utekelezaji wa Dira ya Taifa ya 2050. 

FCC ina utamaduni shirikishi katika kujadili mambo yahusuyo taasisi, ambapo watumishi wote kupitia ngazi mbalimbali hushirikishwa kwa ustawi wa taasisi. 

Kikao hicho kimefanyika Februari 02,2026 katika ukumbi wa Hoteli ya Tiffany Diamond, Jijini Dar es Salaam.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, Bi. Khadija Ngasongwa akizungumza na watumishi wa FCC (hawapo pichani) katika kikao kazi na watumishi wa Tume, kilichofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Tiffany Diamond, Jijini Dar es Salaam Februari 02,2026.
Bw. Shalua Magandi, Mkurugenzi wa Huduma Saidizi akichangia mada wakati wa kikao kazi na watumishi wa Tume, kilichofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Tiffany Diamond, Jijini Dar es Salaam Februari 02,2026.Mwenyekiti wa Tughe Tawi la FCC, Bw. Emmanuel Ndyetabula akifuatilia kikao kazi cha Kaimu Mkurugenzi Mkuu na watumishi wa Tume, kilichofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Tiffany Diamond, Jijini Dar es Salaam Februari 02,2026.


Sehemu ya watumishi.




Picha za pamoja.

Na Nasra Ismail, Geita

Baraza la Madiwani Halmashauri ya Wilaya ya Geita leo Februari 3,2026 katika Mkutano wake wa Kawaida wa robo ya pili kwa mwaka 2025/26 limewasilisha taarifa ya utekelezaji wa shughuli za maendeleo kwa ngazi ya kata.

Awali akizungumza katika baraza Hilo katika Ukumbi wa Mikutano wa Halmashauri uliopo Nzera,  Mkurugenzi Mtendaji Halmashauri ya Wilaya ya Geita Karia Rajab Magaro amewapongeza madiwani  hao kwa kupewa ridhaa na wananchi ili kuendelea kuisimamia Serikali katika utekelezaji wa shughuli za maendeleo kwa mujibu wa  Kanuni,sheria na taratibu zilizowekwa.

"Tufanye kazi kwa kushirikiana ili kuweza kufanikisha shughuli za Halmashauri" Amesema Bw. Magaro.

Vilevile Magaro ametoa wito kwa Waheshimiwa Madiwani kushirikiana na watendaji katika Kata zao kufanya vikao  na kuwa na taarifa za mapato na matumizi kwa ustawi wa Halmashauri.

"Taarifa za mapato na matumizi ni muhimu sana hivyo nitoe wito kwenu kuzisimamia kwa kushirikiana na watendaji" Amesema Bw Magaro. 

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Mkutano huo ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri na Diwani wa Kata ya Nkome Mhe Christopher Kahesi amewataka Madiwani kuwa mfano mzuri kwa kuzingatia na kuzifuata kanuni,  taratibu na miongozo iliyopo ili kuwa na viwango vizuri.

Pamoja na hayo Mhe Kahesi katika Mkutano huo amewasihi Madiwani  kuendelea kutoa  ushirikiano katika kata nyingine ambazo zina changamoto ili  kuzitatua kwa ushirikiano kwa maslahi ya Halmashauri.

Mkutano huo ni wa Kwanza kwa kipindi cha robo ya pili Oktoba hadi Desemba tangu baraza  hilo lilipoingia kazini ambapo jumla ya kata 37 za Halmashauri ya Wilaya ya Geita zimewasilisha taarifa za utekelezaji wa shughuli za maendeleo kwa ngazi ya Kata.














 

 

Na Mwandishi Wetu, Babati – Manyara.

Maafisa Mawasiliano wa Serikali mkoani Manyara wametakiwa kujitathmini, kuimarisha weledi wao na kujipa thamani kazini ili kuongeza ufanisi wa vitengo vya mawasiliano na mchango wake katika utekelezaji wa shughuli za Serikali.

Wito huo umetolewa na Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Manyara, Bw. Dominic Mbwette, wakati wa ufunguzi wa kikao kazi cha siku mbili cha Maafisa Mawasiliano wa Serikali wa Mkoa wa Manyara kilichofanyika jijini Babati kuanzia Februari 2 hadi 3, 2026.

Bw. Mbwette alisema kuwa changamoto ya kutotambuliwa kwa baadhi ya Vitengo vya Mawasiliano ndani ya taasisi za Serikali inaweza kupatiwa suluhisho endapo Maafisa Mawasiliano wenyewe wataonesha kwa vitendo thamani ya taaluma yao kupitia uwajibikaji, ubunifu na matokeo chanya ya kazi wanazofanya.

“Umuhimu wenu hauamuliwi na cheo pekee bali na matokeo ya kazi zenu. Mkijipa thamani kwa kutekeleza majukumu kwa ufanisi, ni rahisi kwa viongozi na jamii kuona mchango wenu,” alisema Mbwette.

Ameongeza kuwa Maafisa Mawasiliano ni nguzo muhimu ya kuimarisha uwazi, kuwajengea wananchi uelewa wa mipango ya Serikali na kukuza imani kati ya Serikali na jamii, hivyo wanapaswa kutumia fursa hiyo kama sehemu ya kujenga taswira chanya ya utumishi wa umma.

Aidha, aliahidi kuwa Ofisi ya Katibu Tawala wa Mkoa itaendelea kutoa miongozo na maelekezo kwa Halmashauri zote ili kuhakikisha Vitengo vya Mawasiliano vinapatiwa rasilimali na bajeti stahiki kwa utekelezaji wa majukumu yao.

Kwa upande wao, Maafisa Mawasiliano walieleza kuwa kikao kazi hicho kimewapa fursa ya kubadilishana uzoefu, kuimarisha ujuzi na kuweka mikakati ya pamoja ya kuboresha utoaji wa taarifa za Serikali kwa wananchi.
Bw. Mbwette alihitimisha kwa kuwataka Maafisa Mawasiliano kuendelea kufanya kazi kwa weledi, uzalendo na nidhamu ili kuimarisha uwajibikaji na uwazi katika utumishi wa umma mkoani Manyara.
Na. Chedaiwe Msuya na Jordan Mbwambo WF, Dodoma.

Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), amesema Serikali inaendelea kuchukua hatua mbalimbali kudhibiti mikopo yenye riba kubwa ili kulinda wananchi dhidi ya mikopo hatarishi, ikiwemo kuimarisha usimamizi wa sekta ya fedha kupitia Benki Kuu ya Tanzania (BoT).

Mhe. Munde alitoa kauli hiyo bungeni jijini Dodoma wakati akijibu swali la Mbunge wa Jimbo la Kigamboni, Mhe. Nyakisa Sanga, aliyetaka kufahamu hatua zinazochukuliwa na Serikali kuhakikisha wananchi, hususan wafanyakazi, hawabebeshwi mzigo wa riba kubwa za mikopo.

Alieleza kuwa Serikali kwa kushirikiana na BoT imeendelea kusimamia kwa karibu taasisi za fedha ili kuhakikisha zinazingatia sheria, kanuni na miongozo ya utoaji wa mikopo.

Akijibu swali la msingi lililoulizwa kuhusu wakati ambao wafanyakazi wa Tanzania watapunguziwa riba za mikopo na kufikia asilimia 7 au 8, Mhe. Munde alisema kuwa kwa mujibu wa sera za uchumi wa nchi, riba za mikopo zinazotolewa na taasisi za fedha huamuliwa na nguvu za soko, hivyo Serikali haiwezi kuelekeza moja kwa moja taasisi hizo kuweka viwango maalum vya riba kwa kundi fulani la wakopaji.

“Riba za mikopo nchini huamuliwa na soko. Serikali ikielekeza taasisi za fedha kuweka kiwango maalum cha riba kwa wafanyakazi au mkopaji yeyote, itakuwa inakinzana na mwelekeo wa sera ya soko huria,” alisema Mhe. Munde.

Mhe. Munde alifafanua kuwa taasisi za fedha zina uhuru wa kuweka viwango vya riba vya chini ikiwemo asilimia 7 au pungufu endapo zitaona inafaa kufanya hivyo.

Aidha, wafanyakazi binafsi au kupitia waajiri wao wana fursa ya kufanya majadiliano na benki husika ili kukubaliana juu ya viwango vya riba vinavyoweza kutolewa.

Mhe. Munde alisisitiza kuwa Serikali itaendelea kuboresha mazingira ya kifedha nchini kwa lengo la kuhakikisha upatikanaji wa mikopo yenye masharti nafuu na yenye tija kwa wananchi, huku ikilinda misingi ya sera ya soko huria inayotumika nchini.

Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb) akitoa ufafanuzi kuhusu hatua zinazochukuliwa na Serikali kudhibiti mikopo yenye riba kubwa (mikopo umiza) wakati akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Jimbo la Kiamboni, Mhe. Nyakisa Sanga, pamoja na swali la msingi kuhusu riba za mikopo kwa wafanyakazi, bungeni jijini Dodoma.(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, WF, Dodoma) 


Top News