Na TAEC Dodoma


Kila mwaka tarehe 29 Agosti, dunia huadhimisha Siku ya Kimataifa ya Kupinga Majaribio ya Nyuklia (International Day against Nuclear Tests), ikiwa ni fursa ya kutafakari madhara yaliyosababishwa na majaribio ya silaha za nyuklia na kuendelea kuhimiza juhudi za kujenga dunia yenye amani na usalama.

Siku hii ilianzishwa na Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa mwaka 2009 kupitia Azimio Na. 64/35, kwa lengo la kuongeza uelewa kuhusu madhara ya majaribio ya silaha za nyuklia na umuhimu wa kuyasitisha. Tarehe 29 Agosti pia ina umuhimu wa kihistoria kutokana na kufungwa kwa eneo la majaribio ya nyuklia la Semipalatinsk nchini Kazakhstan mwaka 1991.

Tangu jaribio la kwanza la silaha ya nyuklia mwaka 1945, zaidi ya majaribio 2,000 yamefanyika duniani, yakiacha historia ya madhara kwa afya ya binadamu, mazingira na usalama wa dunia.

Katika kuadhimisha siku hii, Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania (TAEC) inaungana na jumuiya ya kimataifa kupinga majaribio ya silaha za nyuklia na kusisitiza matumizi salama, yenye uwajibikaji na ya amani ya sayansi na teknolojia ya nyuklia.

Ni muhimu kuelewa kuwa kupinga majaribio ya silaha za nyuklia si kupinga teknolojia ya nyuklia. Teknolojia hii inapotumika kwa madhumuni ya amani na chini ya mifumo madhubuti ya usalama na udhibiti, ina mchango mkubwa katika kuboresha maisha na kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Nchini Tanzania, TAEC ina jukumu la kusimamia na kudhibiti matumizi salama ya vyanzo vya mionzi pamoja na kuhamasisha matumizi ya amani ya teknolojia ya nyuklia katika sekta mbalimbali zikiwemo afya, kilimo, mifugo, viwanda, migodi, maji, utafiti, mazingira na nishati.

Katika afya, teknolojia ya mionzi inatumika katika uchunguzi na matibabu ya magonjwa mbalimbali; katika kilimo na mifugo inachangia katika utafiti, uboreshaji wa uzalishaji na udhibiti wa baadhi ya wadudu na magonjwa. Mbinu za nyuklia pia zina matumizi muhimu katika tafiti za rasilimali za maji, viwanda, migodi na maeneo mengine ya maendeleo.

Kwa msingi huo, tunapaswa kutofautisha kati ya matumizi ya nyuklia kwa madhumuni ya kijeshi na matumizi yake kwa madhumuni ya amani. Hofu inayotokana na madhara ya silaha za nyuklia isiwe sababu ya kuiona teknolojia yote ya nyuklia kama tishio.

TAEC itaendelea kuhakikisha matumizi ya vyanzo vya mionzi nchini yanafanyika kwa kuzingatia sheria na viwango vya usalama ili kuwalinda wafanyakazi, wagonjwa, wananchi na mazingira. Tutaendelea pia kutoa elimu kwa umma ili kuondoa dhana potofu na kuongeza uelewa kuhusu manufaa ya matumizi salama ya teknolojia ya nyuklia.

Tunapoadhimisha Siku ya Kimataifa ya Kupinga Majaribio ya Nyuklia, tunatoa wito kwa wananchi kuendelea kupata taarifa sahihi na kuunga mkono matumizi salama na ya amani ya teknolojia ya nyuklia kwa manufaa ya Taifa na ustawi wa binadamu.

Ujumbe wetu ni wazi: HAPANA kwa majaribio ya silaha za nyuklia; NDIYO kwa matumizi salama na ya amani ya teknolojia ya nyuklia kwa maendeleo ya Taifa.

“Mionzi kwa Matumizi Salama na Teknolojia ya Nyuklia kwa Maendeleo ya Taifa.”

Na Janeth Raphael - MichuziTv -Ikulu Chamwino 

 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema uamuzi wa kumteua Deogratius Ndejembi kuwa Makamu wa Rais ulizingatia sifa, uzoefu na uwezo wake wa kubeba dhamana kubwa ya uongozi wa taifa.

Rais Samia amesema nafasi hiyo imekabidhiwa tena kwa kijana, akimtaka Ndejembi kutumia fursa hiyo kujifunza, kukua kiakili na kutekeleza majukumu yake kwa weledi, utii na uaminifu kwa maslahi ya Watanzania.

Akizungumza leo, Agosti 29, 2026, katika hafla ya kumuapisha Ndejembi kuwa Makamu wa Rais iliyofanyika Ikulu Chamwino, Dodoma, Rais Samia amesema uamuzi wa kumrudisha kijana katika nafasi hiyo ulifanyika kwa kauli moja.

“Kwa kauli moja tuliamua kuirudisha nafasi ya Makamu wa Rais kwa vijana na tuendelee kulea. Imetoka kwa kijana na tumeirudisha kwa kijana. Tunakuomba kijana (Ndejembi) ukakue sio kwa umri bali ukakue kiakili, tumekupa majukumu makubwa ni imani yangu utaweza,” amesema Rais Samia.

Rais Samia amesema Ndejembi alipata uungwaji mkono wa wabunge kwa kauli moja kutokana na sifa alizonazo zinazomfanya astahili kushika nafasi hiyo.

“Wabunge walimpitisha Deogratius Ndejembi kwa kauli moja kwa kuzingatia sifa za Makamu wetu wa Rais,” amesema.

Amesema kabla ya kufikia nafasi ya Makamu wa Rais, Ndejembi amewahi kushika nafasi mbalimbali za uongozi serikalini na katika sekta binafsi, akieleza kuwa uzoefu huo utakuwa nyenzo muhimu katika utekelezaji wa majukumu yake mapya.

“Makamu wa Rais Deogratius Ndejembi, kabla ya wadhifa huu, ulishika nafasi mbalimbali za uongozi serikalini na sekta binafsi. Sina shaka kwamba uzoefu huo utakusaidia kutekeleza majukumu ya dhamana hii uliyopewa,” amesema Rais Samia.

Kwa mujibu wa Rais Samia, hakuna shule maalumu inayomwandaa mtu kuwa Makamu wa Rais, bali uwezo wa kutekeleza majukumu hayo unajengwa kupitia sifa binafsi, bidii, weledi, nidhamu pamoja na utayari wa kujifunza na kusimamia utekelezaji wa majukumu.

Amesema sifa hizo zitamsaidia Ndejembi kutekeleza ipasavyo dhamana aliyopewa na taifa.

Rais Samia pia amesema uzoefu wa Ndejembi ndio uliowafanya viongozi kutokuwa na kusita katika kupitisha jina lake wakati wa kutafuta mtu wa kujaza nafasi hiyo.

“Kwa uzoefu huo ndio maana wakati tunatafuta mtu wa kujaza nafasi hii, hatukusita hata kidogo kupitisha jina lako. Hivyo ni matamanio na matarajio yetu sote Watanzania utalitumikia vyema, kwa utii, uaminifu, utu, busara, uzalendo, hekima, maarifa na uzoefu ulio nao, ukimtanguliza Mungu mbele na kwa maslahi ya taifa,” amesema.

Katika hatua nyingine, Rais Samia amemtaka Ndejembi kwenda kuwatumikia Watanzania wote bila kujali tofauti zao, akisisitiza umuhimu wa kiongozi kuweka mbele maslahi ya taifa.

“Nenda ukawatumikie Watanzania bila kujali tofauti zao,” amesema Rais Samia.

Rais Samia amesema serikali ina kazi kubwa ya kutekeleza ahadi zilizowekwa kupitia Ilani ya Chama cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2025–2030, sambamba na kuanza utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya miaka 25 ijayo.

Amesema dira hiyo imebeba matarajio makubwa ya maendeleo kwa wananchi, hivyo utekelezaji wake unahitaji umoja, mshikamano, ushirikiano, utulivu na uongozi bora.

“Ili tuweze kutekeleza haya yote kwa maslahi ya wananchi wetu na taifa kwa ujumla, tunahitaji umoja, mshikamano, ushirikiano, utulivu na uongozi bora,” amesema.

Uapisho wa Ndejembi unafungua rasmi ukurasa mpya katika safari yake ya uongozi wa kitaifa, huku akianza kutekeleza majukumu ya Makamu wa Rais chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan


















 


RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema ni matamanio na matarajio ya Watanzania wote kwamba Makamu wa Rais, Deogratius Ndejembi, ataitumikia vyema Tanzania kwa utii, uaminifu, utu, busara, hekima, uzalendo na maarifa

Rais Samia ameyasema hayo leo Jumamosi, Agosti 29, 2026, Ikulu ya Chamwino, Dodoma, mara baada ya kumuapisha Ndejembi kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Amesema uteuzi wa Ndejembi umetokana na kuzingatia sifa na vigezo alivyo navyo, ikiwemo umri wake ambao, kwa mujibu wa Rais Samia, bado ni kijana mwenye nguvu, ari na kasi ya kujituma katika kutekeleza shughuli za Serikali.

“Nivishukuru vikao vya Chama cha Mapinduzi vya Kamati Kuu na Halmashauri Kuu kwa kupendekeza na kuridhia jina la Deogratius Ndejembi katika nafasi ya Makamu wa Rais,” amesema Rais Samia.

Amesema kwa kauli moja waliamua kuirudisha nafasi hiyo kwa vijana ili waendelee kulelewa katika uongozi, akimtaka Ndejembi akue kiakili kutokana na ukubwa wa majukumu aliyopewa.

Rais Samia amesema Ndejembi ana uzoefu wa uongozi serikalini na sekta binafsi, hivyo anaamini uzoefu huo utamsaidia kutekeleza majukumu ya dhamana hiyo.

“Cheo ni dhamana, cheo hiki tulichokupa sio ufalme ni dhamana. Ni dhamana uliyopewa na Watanzania kupitia Chama cha Mapinduzi lakini pia kupitia Bunge,” amesema.

Ametoa wito kwa Ndejembi kuwatumikia Watanzania bila kujali tofauti zao, huku akisisitiza umuhimu wa umoja, mshikamano, ushirikiano, utulivu na uongozi bora katika kutekeleza Ilani ya CCM ya 2025–2030 na Dira ya Maendeleo ya miaka 25 ijayo.

Rais Samia pia amewashukuru mabalozi na wakuu wa mashirika ya kimataifa waliohudhuria tukio hilo, akisema uwepo wao unaonesha urafiki, udugu na ushirikiano na Tanzania, pamoja na ushahidi wa uwezo wa nchi kubadilisha viongozi kwa amani na utulivu.



Na Lusungu Helela, Dodoma 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhwani Kikwete, amesema uamuzi wa Serikali ya Somalia kumtuma Waziri mwenye dhamana ya Utumishi wa Umma nchini Tanzania ni ishara ya kutambua mafanikio yaliyofikiwa na Tanzania katika eneo la matumizi ya mifumo katika masuala ya Utumishi wa Umma nchini. 

Mhe. Kikwete amesema hayo leo jijini Dodoma wakati akizungumza na ujumbe wa Serikali ya Somalia unaoongozwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Masuala ya Utumishi wa Umma, Hirsi Jama Ganni, uliofika nchini kwa ziara ya kikazi ya siku tatu. 

Amesema ujio wa ujumbe huo unaonyesha kuwa Somalia inatambua na kuthamini uzoefu wa Tanzania katika uendeshaji wa Serikali, utumishi wa umma na matumizi ya mifumo ya kidijitali katika utoaji wa huduma kwa wananchi. 

“Ukiona wenzako wanakufuata hasa katika eneo hili ambalo sisi ni watoa huduma, ni wazi kuwa huduma tunayotoa wapo wenzetu wanatambua na kuthamini tunachokifanya na ndiyo maana wameamua kuja kujifunza na kupata uzoefu,” amesema Mhe. Kikwete 

Amesema anaamini uzoefu ambao Somalia itaupata kupitia ziara hiyo utasaidia kuboresha zaidi masuala ya utumishi wa umma nchini humo. 

Mhe. Kikwete amesema ujumbe huo unapata fursa ya kujifunza maeneo mbalimbali, ikiwemo namna Serikali inavyohusiana na wananchi, uratibu wa masuala ya kazi na ajira, usalama wa wafanyakazi mahali pa kazi pamoja na mifumo ya pensheni kwa watumishi wanaostaafu katika taasisi za Serikali na sekta binafsi. 

“Hii ziara ni kielelezo tosha kuwa Somalia imedhamiria, ndiyo maana haijaweza kutuma maafisa pekee, lakini Waziri mwenye dhamana ya Utumishi wa Umma ameamua kuja mwenyewe na timu yake kwa lengo la kujifunza na kuja kuona kwa macho yake kazi kubwa iliyofanyika Tanzania,” amesisitiza Mhe. Kikwete 

Kwa upande wake, Mhe. Ganni amesema ujumbe wake umefika Tanzania kujifunza namna Tanzania ilivyofanikiwa katika masuala ya utumishi wa umma, hususan matumizi ya mifumo ya kidijitali katika kuboresha utoaji wa huduma. 

Amesema Tanzania imekuwa ikifanya vizuri katika utoaji wa huduma kwa wananchi, huku watumishi wa umma wakitumia mifumo ya kidijitali kuwahudumia wananchi na kuhakikisha wanapata haki zao. 

Mhe. Ganni amesema ujio wao ni muhimu kutokana na hatua ambazo Tanzania imepiga katika kuboresha utendaji wa Serikali na utoaji wa huduma kwa wananchi. 

Amesema wamevutiwa pia na namna mifumo ya Serikali inavyowawezesha watumishi kuwahudumia wananchi kwa ufanisi. 

Akizungumzia mfumo wa e-Mrejesho, Mhe.Ganni amesema ni miongoni mwa mifumo waliyoona ina umuhimu katika kuimarisha mawasiliano kati ya Serikali na wananchi, hivyo wanatarajia kujifunza namna unavyofanya kazi na uwezekano wa kutumia uzoefu huo katika kuboresha huduma nchini Somalia. 

Ziara hiyo ya ujumbe wa Somalia inalenga pia kujifunza kuhusu mifumo ya Baraza la Mawaziri, usimamizi wa rasilimali watu, uajiri kwa kuzingatia sifa, Serikali mtandao, usimamizi wa ajira na mifumo ya taarifa za soko la ajira. 

Ujumbe huo pia unatarajiwa kutembelea Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Mahusiano pamoja na Mji wa  Serikali Mtumba jijini Dodoma, kwa ajili ya kujionea namna shughuli za Serikali zinavyoratibiwa na kutekelezwa.














 

Wanachama waliohitimu pamoja na familia zao kwenye mahafali ya Awamu ya Pili, Mapigano, Ulyankulu, tarehe 21 Agosti 2026.

Mradi wa DREAMS Tanzania ulianza ukiwa na lengo la kuthibitisha kwamba kaya maskini zaidi zinaweza kujenga biashara zinazodumu. Ndani ya siku nne za mwezi Agosti, kaya 1,356 zilizohitimu zilitoa ushahidi.


ULYANKULU, MKOA WA TABORA, TANZANIA · AGOSTI 2026.

Mwezi Februari 2025, maafisa wa mradi walipita nyumba kwa nyumba katika vijiji vinne vya eneo hili la mkoa wa Tabora. Walikuta kwamba asilimia 14 tu ya kaya maskini zaidi zilikuwa zinaishi kwa zaidi ya dola tatu kwa siku. Baada ya miezi 12 ya utelekelezaji wa mradi, idadi hiyo ilikuwa imefika asilimia 82.75.

Mahafali mawili yaliyotenganishwa na siku tatu yalionesha mabadiliko hayo. Chini ya hema pale Mapigano siku ya Ijumaa tarehe 21 Agosti, kaya 762 kutoka Mbeta, Mapigano na Taba zilipokea vyeti vyao kutoka kwa Jumanne Singani, mkuu wa makazi ya Ulyankulu. Pale Sasu siku ya Jumatatu tarehe 24 Agosti, kaya nyingine 594 zilipokea vyao, huku Mkuu wa Wilaya ya Kaliua akiwa mgeni rasmi. Viongozi wa vikundi walipanda mmoja mmoja kupeana mikono mezani kuu, kuchukua cheti na kusimama kwa ajili ya picha. Kwaya ziliimba, vikundi vya biashara vilitandika mazao, kuku na mchele uliokobolewa, na kila mradi ulipotajwa umati ulijibu jambo lilelile: ongeza kipato cha familia.

Jumanne Singani, mkuu wa makazi ya Ulyankulu na mgeni rasmi, akizungumza na wahitimu kutoka meza kuu pale Mapigano.

Kwa pamoja kaya hizo 1,356 ndio Awamu ya Pili, na zote ziliingia kwenye mradi zikiwa miongoni mwa kaya maskini zaidi ndani ya makazi. Mradi huu unaitwa DREAMS Tanzania, na upo ili kujibu swali ambalo mashirika ya maendeleo yameshughilika nalo kwa miongo mingi: je, familia zilizo kwenye umaskini uliokithiri zinaweza kuingizwa kwenye uchumi wa kudumu, au msaada huishia kupotea tu mara mradi unapoondoka?

DREAMS, au Delivering Resilient Enterprises and Market Systems, unaongozwa na Mercy Corps kwa kushirikiana na Village Enterprise, Caritas Tabora na shirika la msaada wa kisheria la Dignity Kwanza. Utaendelea hadi Desemba 2027, unalenga kujenga uwezo wa kujitegemea kwa watu 150,000 katika makazi ya Ulyankulu, Mishamo na Katumba pamoja na vijiji vinavyozunguka hayo makazi, ambako Watanzania waliopewa uraia na vijiji vinavyowazunguka wanaishi bega kwa bega. Hadi sasa umewafikia watu 140,414.

JINSI MRADI UNAVYOFANYA KAZI

Mbinu yenyewe ni ya polepole kwa makusudi. Hakuna anayekabidhiwa pesa siku ya kwanza. Maafisa hupita kwanza kila kaya katika kijiji kilichochaguliwa wakiwa na dodoso la kupima hali ya umaskini, Poverty Probability Index (PPI), na majibu ndiyo yanayoamua nani anastahili. "Hatukai chini ya mti na mwenyekiti tukamuuliza nani maskini hapa," anasema January Julius Nyanda, anayesimamia timu za uwandani kwa upande wa Caritas Tabora. "Angetutajia majina ya ndugu zake wote."

Katika Awamu ya Pili, kaya 1,670 zilikidhi vigezo na kaya 1,356 zikajiunga. Zilipitia mada tisa za mafunzo kuhusu uendeshaji wa vikundi, elimu ya fedha na ujasiriamali, kisha zikaunda vikundi vya kuweka akiba na kukopeshana vya wanachama thelathini hadi arobaini na tano, pamoja na vikundi vya biashara vya kaya tatu tatu. Ndipo pesa ilipofika: shilingi 533,820 kwa kila kikundi, na mgao wa pili wa shilingi 228,720 baada ya miezi sita, jumla ya shilingi milioni 344.4 katika biashara 452.

Kikundi cha biashara kikionesha bidhaa zake kwenye mahafali: miche ya sabuni, sahani zilizopangwa, nyanya na kabichi.

Fredrick Kumbule Modestus, aliyewashauri takribani washiriki 150, anakumbuka waziwazi walipoanzia. "Mtu alikuwa anapata shilingi elfu kumi bila kuwa na wazo kwamba angeweza kutumia elfu saba na kubakiza elfu tatu," anasema. "Wazo la biashara halikuwepo kabisa."

Si kila mtu alijiunga mwanzoni. Zilienea tetesi kwamba mtaji ungerudishwa baadaye, kwa ardhi au kwa mifugo, na baadhi walikaa pembeni mpaka walipoona vikundi vya kwanza vikinufaika.

MWAKA MMOJA UMEZAA NINI

Utafiti wa mwisho, uliofanywa na Caritas Tabora awamu ilipomalizika, ulionesha wastani wa mali za kaya umepanda kutoka dola 260 hadi dola 955, na matumizi kwa kila mtu kutoka dola 164 hadi dola 453. Kaya zinazoweka akiba mara kwa mara zilipanda kutoka asilimia 3.5 hadi asilimia 99.7, na asilimia 91.8 ya biashara zilipimwa kuwa zenye afya wakati wa kuhitimu.

John Brighton Mwangolela ni mkulima wa kitongoji cha Itagwa, kilichoko Sasu. Kwenye mahafali ya Jumatatu alizungumzia mafanikio waliyopata katika kikundi chao;

"Tulianza na mbuzi wanne. Mwisho wa mwaka tukawa na mbuzi kumi na sita. Tukagawana mbuzi mmoja mwenye mimba kila mmoja, na wale kumi na watatu waliobaki tukawauza tukanunua ng'ombe jike mwenye mimba. Hivi ninavyosimama hapa, ana wiki tangu amezaa, na sasa tunakunywa maziwa yake."
John Brighton Mwangolela
Mhitimu, kitongoji cha Itagwa, Sasu

Antonet Yohana ni mwenyekiti wa kikundi cha kuweka akiba cha Muungano kilichoko Taba, ambacho hununua mpunga, hukikoboa na kuuza mchele kwa kupima. Mwezi aliouchagua ni Januari, wakati ada za shule zinapofika na wazazi walipokuwa wanakopa kwa wenye pesa kwa riba aliyoiita nusu kwa nusu. Sasa kikundi chake kinawakopesha wanachama wake wenyewe kwa riba nafuu.

SHERIA ILIBADILISHA NINI

Pesa huleta matatizo yake yenyewe, na ndiyo maana shirika la msaada wa kisheria lipo ndani ya muungano huu wa mashirika. Ulyankulu ni ardhi tengefu na haiwezi kununuliwa wala kuuzwa ndani ya makazi, hivyo kipato kinapopanda ni lazima kiambatane na uelewa wa mahali ambapo ardhi inaweza kununuliwa kihalali. Masala Johnson, afisa wa masuala ya kisheria wa mradi, pia amewasaidia wanachama kupata vyeti vya kuzaliwa kwa watoto wanaojiunga na kidato cha tano, na namba za utambulisho wa taifa, ambazo bila hivyo hakuna akaunti ya benki inaweza kufunguliwa.

Timu yake ilifanya kazi kwenye mazingira magumu. "Awali tulipoingia kwenye mradi huu, kulikuwa na matukio mengi ya ukatili wa kijinsia yakiripotiwa ndani ya nyumba, ikiwemo wanaume kutowaruhusu wake zao kuhudhuria mafunzo ya biashara," anasema. "Sasa wapo wanaume wanaotoa ushuhuda kwamba wamewaruhusu wake zao kufanya biashara."

Kwa Mwangolela, masomo ya sheria yalibadilisha namna kijiji chake kinavyozungumzia mabinti.

"Akizaliwa mtoto wa kiume tulisema tumepata mchungaji wa mifugo, na akizaliwa wa kike tulisema tumepata mahari kubwa. DREAMS walitufundisha sheria na wakatufundisha madhara yake. Nenda Itagwa sasa. Shule yetu imejaa watoto kwa sababu ya DREAMS."
John Brighton Mwangolela

MASOKO YENYE SABABU ZAKE ZA KUBAKI

Kinachotofautisha DREAMS na mradi wa kugawa ruzuku ni kinachotokea pale biashara zinapokuwa zimeshaanza. CRDB Bank Foundation ilihamisha pesa kutoka kwenye masanduku na kuiingiza kwenye akaunti takribani 708 katika eneo la Ulyankulu pekee, KickStart International inasambaza pampu za umwagiliaji, SimuSolar inatoa mashine za kusaga na za umwagiliaji zinazotumia nishati ya jua kwa mkopo usio na riba, na AKM Glitters inatoa vifaranga vya siku moja. Mgarang'ombe Traders, wanaokoboa mpunga, walijiunga ili kuimarisha mnyororo wa thamani wa zao la mpunga, nao wakapata kitu.

"Mimi ni mfanyabiashara wa muda mrefu, lakini nilikuwa sina elimu ya biashara. DREAMS walitufundisha, na wakatuomba tuwafikishie wakulima tunaowanunulia mazao. Sasa wanazalisha mchele bora kabisa wa grade A na grade B."
Peter Maganga Mapembe
Wakala, Mgarang'ombe Traders, kata ya Makingi

Kwa mradi mzima, kila dola moja ambayo DREAMS inawekeza imeambatana na dola 4.83 za mtaji wa sekta binafsi.

Kikundi bora cha kuweka akiba katika kila kijiji kilipewa viti hamsini vya plastiki badala ya pesa taslimu, kwa sababu katika vijiji, kila harusi na kila msiba unahitaji viti, viti vinaweza kukodishwa.

KINACHODUMU

Hata zawadi zilibeba mantiki ya mradi. Ili kikundi kistahili kupata viti, kila mwanachama alipaswa kuwa ameweka akiba isiyopungua shilingi 250,000 katika mzunguko wa wiki 52. Pale Sasu zawadi ilikwenda kwa kikundi cha Maboresho, kilichokuwa kimeweka shilingi 12,882,000.

Vyeti vina uzito zaidi. DREAMS hufanya kazi kupitia viongozi wa wilaya badala ya kuwazunguka, na pale Sasu Mkuu wa Wilaya ya Kaliua aliwaambia wahitimu kwamba halmashauri hutenga asilimia kumi ya mapato yake kwa ajili ya mikopo ya vikundi, akiwaagiza watumishi wake kuvipa kipaumbele vikundi vyenye vyeti vya DREAMS. "Cheti hicho kimesajiliwa na halmashauri na kinatambulika nayo," Martin Mgallah, meneja msaidizi wa mradi, aliwaambia. "Wenyeviti, kitunzeni. Ndiyo uhai wa kikundi chenu."

Martin Mgallah, meneja msaidizi wa mradi wa DREAMS Tanzania.

Sehemu nyingine za mpangilio wa mradi zinaelekea upande huohuo. Vikundi vya kuweka akiba vinamilikiwa na wanachama wenyewe na havihitaji pesa kutoka nje ili viendelee kufanya kazi, kila biashara ni mali ya kaya tatu badala ya kaya moja, na maafisa wa wilaya wanashikilia kumbukumbu za kila kikundi.

Awamu ya Kwanza ndiyo mtihani halisi wa kwanza. "Tuliwaaga mwaka mmoja uliopita," alisema Mgallah. "Tumetembelea biashara zao jana. Bado wanafanya biashara na wanaendelea kufanikiwa." Mmoja wao ni Abraham Mgaywa wa Makingi, aliyekuwa na familia kubwa na hakuwa na kipato cha kukidhi mahitaji yake wakati dodoso lilipomfikia. Sasa anajiita Mabala the Farmer, na mwezi huu amesafirisha maroli mawili ya matikiti kwenda Dodoma wakati bei ilipokuwa juu kabisa.

Awamu nyingine nne zinaendelea na mafunzo nyuma ya Awamu ya Pili, jumla ya kaya 5,245, na mwakani maafisa watakuwa milangoni Mkindo, Makonge, Kaswa, Usigara, Keza na Ikonongo. Obed Method Bujoro, mwenyekiti wa serikali ya kijiji cha Mapigano, anataka warudi kijijini kwake. Ameona jambo ambalo hakuna utafiti ungeliweza kuligundua: watoto wa kaya zenye shida walikuwa wakitokea milangoni kwa majirani wakati wa chakula, na hilo limekoma.

Wahitimu na watumishi wa DREAMS wakicheza mwishoni mwa mahafali.

Anastazia Paulo Makula alisoma risala ya wahitimu pale Sasu. Alijiunga bila mtaji wowote, akajiwekea lengo la kuweka akiba kwa muda wa miezi mitatu, na kwa pesa iliyopatikana akafungua duka la nguo za watoto. Muhtasari wake ndio uliokuwa mfupi kuliko yote siku hiyo.

"Tulikuwa na maisha ya chini sana. Leo nina imani sisi wana Sasu tuko vizuri."
Anastazia Paulo Makula
Kikundi cha kuweka akiba cha Maboresho, Sasu Centre

Mradi wa DREAMS Tanzania unatekelezwa na Mercy Corps kwa kushirikiana na Village Enterprise, Caritas Tabora na Dignity Kwanza, pamoja na wadau wa sekta binafsi wakiwemo CRDB Bank Foundation, Mgarang'ombe Traders, AKM Glitters, SimuSolar na KickStart International.



Na OWM (KAM) Dar es Salaam

Serikali imesema itaendelea kuhakikisha vijana nchini wanaendelea kunufaika na fursa za nje ya nchi na zenye staha kwa kushirikiana na wadau wa ndani na nje ya nchi.

Akizungumza jijini Dar es Salaam Agosti 27,2026 wakati wa uzinduzi wa mkopo wa Ughaibuni Loan unaoratibiwa na Benki ya CRDB pamoja na kuwaaga vijana 130 kati ya 530 wanaotarajia kwenda kufanya kazi nje ya nchi, Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano, Dkt. Evaline Munisi amesema Serikali inatambua ajira za nje ya nchi kama nyenzo muhimu ya kupanua fursa za ajira, kuongeza kipato cha vijana, kukuza ujuzi na kuwajengea uzoefu wa kimataifa.

“Matokeo ya jitihada hizi yamewezesha Watanzania 14,613 kupata ajira nje ya nchi tangu Serikali ya Awamu ya Sita kuingia madarakani. Kati ya Julai 2025 hadi sasa, Watanzania 8,428 wameunganishwa na waajiri nje ya nchi,” amesema Dkt. Munisi.

Amesema mafanikio hayo yameifanya Tanzania kuendelea kuaminika kuwa na nguvu kazi salama na yenye staha duniani.

Kuhusu uzinduzi wa Ughaibuni Loan, Dkt. Munisi amesema mkopo huo unalenga kuwawezesha vijana waliopata ajira nje ya nchi kupata fedha nafuu za kugharamia maandalizi ya safari ikiwemo tiketi ya ndege, bima na visa.

“Ughaibuni Loan siyo msaada bali ni mkopo wa uwezeshaji. Nawasihi vijana wahakikishe wanafanya marejesho ili na wengine wapate fursa,” amesisitiza.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa CRDB, Bw. Pendason Philemon amesema benki imetenga jumla ya Shilingi bilioni 250 kwa miaka mitano kutoa mikopo ya kati ya Sh. 500,000 hadi milioni 20 kwa kila kijana kulingana na gharama za kufika kwa mwajiri wake.

“Kigezo muhimu ni kuwa na mkataba au barua ya ajira iliyothibitishwa na wakala. Marejesho yatakuwa kwa miezi 24 na tunatoa kipindi cha neema cha miezi 2 kwa riba ya asilimia 15,” amesema Philemon.

Mwenyekiti wa Chama cha Mawakala Binafsi wa Ajira TRAA, Bw. Abdala Khalid amesema mkopo huo utawaepusha vijana na watu wasio na nia njema.

Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano, Bi. Zuhura Yunus amesema Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi,Ajira na Mahusiano inaendelea kutafuta masoko ya uhakika ya ajira ikiwemo Saudi Arabia, Oman, Qatar, Denmark na Ujerumani.

Mmoja wa wanufaika, Dickson Tadeo Mbaga amesema kupitia mkopo huo aliweza kugharamia visa, tiketi na bima. “Ninawasihi vijana wenzangu wachangamkie fursa hii,” amesema.

Serikali imesema itaendelea kuhakikisha vijana 530 wanaokwenda kufanya kazi ughaibuni katika fani mbalimbali ikiwemo ujenzi wanalindwa na kazi zao zinakuwa zenye staha.






 


Top News