Dkt. Maghembe azindua Kongamano la Vijana wa Kitanzania chini ya Umoja wa Mataifa (TIMUN 2026) asisitiza umuhimu wa nafasi vijana katika kuleta Maendeleo Endelevu Kitaifa na Ulimwenguni

Leo tarehe 18 Mei 2026, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Ngwaru Jumanne Maghembe (Mb) amemwakilisha Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb), Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwenye uzinduzi wa Kongamano la Vijana wa Kitanzania chini ya Umoja wa Mataifa (Tanzania International Model United Nations -TIMUN 2026)  linalofanyika Zanzibar. Katika Hotuba yake, Mhe. Naibu Waziri Dkt. Maghembe amesisitiza umuhimu wa nafasi ya vijana katika kuleta maendeleo endelevu na mabadiliko chanya, kupitia teknolojia, diplomasia na ubunifu katika ngazi na Taifa na Ulimwenguni.

Mkutano wa TIMUN 2026, ni jukwaa muhimu la kimataifa linalolenga kukuza viongozi vijana, wanadiplomasia, wabunifu, na mawakala wa mabadiliko ambalo hufanyika kila mwaka chini ya uratibu wa Chama cha Vijana katika Umoja wa Mataifa Tanzania  (Youth of United Nations Association Tanzania-YUNA).

Mhe. Maghembe ameipongeza YUNA Tanzania kwa kuwawezesha vijana na kuendeleza maadili ya Umoja wa Mataifa miongoni mwa vijana wa Tanzania na Afrika kwa ujumla.

"Tumieni mkutano huu kubadilishana mawazo, kujenga ushirikiano, na kuibua suluhisho za changamoto mbalimbali zikiwemo mabadiliko ya tabianchi, ukosefu wa ajira, usawa wa kijinsia, na maendeleo ya teknolojia" alibaibisha Mhe. Maghembe












Na Mwandishi wa OMH

Dar es Salaam. Ofisi ya Msajili wa Hazina imekutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa China nchini Tanzania, Chen Mingjian, pamoja na ujumbe wake, katika kikao kilicholenga kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi, uwekezaji na mageuzi ya mashirika ya umma.

Mazungumzo hayo yalifanyika jijini Dar es Salaam Jumatatu, Mei 18, 2026, kati ya menejimenti ya Ofisi ya Msajili wa Hazina ikiongozwa na Msajili wa Hazina, Nehemiah Mchechu, na ujumbe wa Ubalozi wa China ulioongozwa na Balozi wa China nchini Tanzania, Chen Mingjian.

Katika kikao hicho, pande hizo mbili zilijadili masuala ya uwekezaji wa serikali, usimamizi wa kampuni za umma na miradi ya kimkakati.

Akizungumza katika kikao hicho, Bw. Mchechu alisema Ofisi ya Msajili wa Hazina ina jukumu la kusimamia uwekezaji wa serikali katika taasisi na kampuni 308, ambapo 252 kati yake serikali ina hisa nyingi.

Alibainisha kuwa thamani ya uwekezaji wa serikali katika taasisi na kampuni hizo ni Sh92.3 trilioni.

Alisema uwekezaji huo unahusisha sekta mbalimbali zikiwemo usafiri wa anga, nishati, mafuta na gesi na madini, akisisitiza kuwa serikali inaendelea na mwelekeo wa kuongeza ufanisi na uhimilivu wa kifedha katika mashirika hayo.

Kwa upande wake, Balozi wa China nchini Tanzania, Chen Mingjian, alisema China itaendelea kuimarisha ushirikiano na Tanzania katika sekta za uwekezaji, miundombinu na mageuzi ya kiuchumi, akibainisha kuwa uhusiano wa nchi hizo mbili umejengwa katika msingi imara wa miaka mingi ya urafiki na imani ya kisiasa.

Balozi Chen aliongeza kuwa China itaendelea kusaidia jitihada za Tanzania katika kuendeleza viwanda, kuongeza thamani ya rasilimali za madini, pamoja na kuimarisha ushirikiano katika mafunzo na uhamishaji wa teknolojia kwa watumishi wa umma.

Aidha, alieleza kuwa China itaendelea kuunga mkono miradi ya kimkakati inayotekelezwa kwa ushirikiano kati ya nchi hizo mbili, ikiwemo sekta ya usafirishaji, nishati na uwekezaji wa pamoja katika kampuni za kimkakati.






Mwenyekiti wa UWT Taifa, Ndg. Mary Pius Chatanda (MCC), amewasha moto wa kampeni katika kata za Migoli na Kihorogota, kuelekea Uchaguzi Mdogo wa Jimbo la Ismani utakaofanyika tarehe 1 Juni, 2026.

Akizungumza na makundi mbalimbali ya wanawake na wananchi kwa ujumla, Ndg. Chatanda amebainisha kuwa CCM imeonyesha imani kubwa kwa kuweka mgombea mwanamke Ndg. Emmanuela Mtatifikolo Kaganda na sasa ni jukumu la wanawake wote kuungana na kushirikiana ili kupata ushindi.

Pia amepongeza ushirikiano mkubwa na uungwaji mkono kutoka kwa wanaume wa Ismani ambao wameonyesha nia ya dhati ya kumlinda na kumsaidia mgombea wetu ashinde.

Aidha, amewakumbusha kuwa Serikali imara ya awamu ya sita chini ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan tayari ipo madarakani na inafanya kazi kubwa. Uchaguzi huu mdogo ni kwa ajili ya kupata mwakilishi bora atakayeenda kuendeleza mazungumzo ya kimaendeleo ya Ismani bungeni.















CHANGAMOTO ya afya ya akili imetajwa kuwa miongoni mwa matatizo makubwa yanayowakabili walinda amani wanaopelekwa katika misheni za kimataifa, wakiwemo kutoka Tanzania.

Mkuu wa Chuo cha Mafunzo ya Ulinzi wa Amani Tanzania (TPTC), Brigedia Jenerali George Itang’arealisema hayo jijini Dar es Salaam wakati wa ufunguzi rasmi wa programu mbili za kimataifa za mafunzo zilizolenga kuimarisha huduma za kitabibu na msaada wa kisaikolojia kwa walinda amani wanaofanya kazi katika mazingira yenye changamoto kubwa za kiusalama duniani.

Kozi hizo maalumu zinazojikita katika msaada wa kisaikolojia na uimarishaji wa uwezo wa kitabibu, zimewakutanisha wanajeshi, wataalamu wa afya na wakufunzi kutoka mataifa mbalimbali yakiwemo Canada, Rwanda, Cameroon, Indonesia, Urusi, Ujerumani na Marekani, hatua inayoonesha ushirikiano wa kimataifa katika juhudi hizo.

Brig. Gen. Itang’are alisema mtaala huo umeandaliwa mahsusi kuongeza uwezo wa walinda amani kutambua na kushughulikia changamoto kubwa za afya ya akili na matibabu wanazokutana nazo katika maeneo ya operesheni za mbele.

“Tumegundua kupitia uzoefu wa vikosi vya hivi karibuni kuwa kuna uhitaji mkubwa wa mafunzo ya aina hii kwa sababu walinda amani wanafanya kazi katika mazingira yenye msongo mkubwa unaoathiri afya ya akili na ustawi wa kijamii,” alisema.

“Ikiwa huna watumishi wenye afya njema, inakuwa vigumu kufikia ufanisi wa kiutendaji. Ndiyo maana mpango huu ni muhimu.”

Kamanda huyo alisema tathmini za hivi karibuni zilizofanywa katika operesheni za ulinzi wa amani zimebaini mapungufu makubwa katika huduma za msaada wa kisaikolojia na maandalizi ya kitabibu, hali iliyolazimisha kituo hicho kupanua kwa haraka programu zake maalumu za mafunzo.

Sehemu ya mafunzo ya kitabibu itatumia mfumo wa mafunzo kwa wakufunzi (training-of-trainers) ili kuimarisha mifumo ya afya kwa muda mrefu na kuongeza utayari wa kiutendaji kwa wanajeshi kabla na wakati wa misheni za kimataifa.

Wachambuzi walisema ushiriki wa wataalamu kutoka mataifa mbalimbali unaonesha kuongezeka kwa mwafaka wa kimataifa kuhusu umuhimu wa ushirikiano wa pande nyingi katika kulinda rasilimali watu inayobeba shughuli za ulinzi wa amani duniani.

Dkt. Annie Swai, mkufunzi mkuu wa afya ya akili na msaada wa kisaikolojia katika TPTC, alisema afya ya akili bado ni moja ya sekta zisizoeleweka vizuri katika huduma za afya licha ya athari zake kubwa katika mazingira ya kazi ya kijeshi.

Alionya kuwa matatizo ya kisaikolojia yasipotibiwa huendelea kuwa mabaya zaidi kadri muda unavyokwenda, hali inayopunguza uwezo wa utendaji kazi, kudhoofisha majukumu ya kijamii na kuyumbisha mshikamano wa taasisi.

Dkt. Swai alisema mazingira yenye presha kubwa katika misheni za ulinzi wa amani huwafanya wengi kubeba kimya kimya msongo mkali wa mawazo, wasiwasi na majeraha ya kihisia, hasa pale ambapo mifumo ya msaada wa taasisi haipo au haifikiki kwa urahisi.

"Changamoto za afya ya akili ni za kawaida na zinatibika, lakini watu wanahitaji mazingira salama ya kuzungumza waziwazi na kutafuta msaada bila hofu,” alisema.

Ili kushughulikia changamoto hizo kwa muda mrefu, Dkt. Swai alisema kituo hicho kinatarajia kuingiza rasmi mafunzo hayo katika mfumo wake wa kudumu wa mafunzo.

TPTC imejipanga kutoa mafunzo hayo angalau mara tatu kwa mwaka kwa lengo la kujenga uimara wa kisaikolojia kwa walinda amani kutoka mataifa yote yanayochangia vikosi vya ulinzi wa amani.







Jeshi Polisi mkoani Arusha limesema kwa kipindi cha kuanzia Aprili 18, 2026 hadi sasa, watuhumiwa 176 wamehukumiwa vifungo mbalimbali kwa makosa ulawiti, ubakaji, wizi, dawa za kulevya, kujeruhi, uvunjaji, kupatikana na nyara za serikali na kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu baada ya kufikishwa Mahakamani. 

Akitoa taarifa hiyo leo Mei 18, 2026 Kamanda wa Polisi Mkoani humo, SACP Justine Masejo amesema kati ya waliohukumiwa kwa makosa makubwa, mtuhumiwa 01 alihukumiwa kunyongwa hadi kufa kwa kosa la mauaji huku mtuhumiwa 01 akihukumiwa kifungo cha maisha gerezani kwa kosa la kulawiti, 

Ameendelea kufafanua kuwa watuhumiwa 02 walihukumiwa miaka 30 gerezani kwa makosa ya kubaka na wizi na watuhumiwa wengine 02 walihukumiwa miaka 20 gerezani kwa makosa ya unyang’anyi wa kutumia silaha na kupatikana na nyara za serikali.

Aidha, amebainisha kuwa kupitia operesheni dhidi ya dawa za kulevya, walifanikiwa kukamata watuhumiwa 19 wakiwa na Mirungi Kilogramu 90 na watuhumiwa 12 wakiwa na bhangi misokoto 177.

Pia kwa kipindi hicho walifanikiwa kukamata Watuhumiwa 33 wakiwa na Pombe ya moshi lita 434 na mitambo 09 ya kutengeneza pombe hiyo.

SACP Masejo amesema operesheni hizo zinaendelea kufanyika maeneo yote katika mkoa huo, ambapo amewataka baadhi ya watu wachache wanaojihusisha na vitendo vya kihalifu kuacha mara moja vitendo hivyo kwani watawakamata na kuchukua hatua za kisheria dhidi yao.

Sambamba na hilo, wataendelea kuchukua hatua kwa madereva wachache wanaoendesha vyombo vya moto kwa kutofuata sheria za usalama barabarani hususani mwendokasi, ulevi na kupita magari mengine bila kuchukua tahadhari.

Jeshi la Polisi mkoani humo limewapongeza wananchi wote wanaotoa taarifa za uhalifu na wahalifu katika maeneo yao hususani katika kipindi hiki kuelekea msimu mkubwa wa utalii katika Mkoa huo.



Na Anne Robi, Mtwara.

WANAFUNZI wa Majukwaa ya sekta ya mafuta na Gas (Oil and Gas Clubs) Mkoani Mtwara wameliomba Shirika la Maendeleo ya Petroli nchini  (TPDC) kuwaandalia ziara ya kutembelea miradi ya gesi asili kujifunza  kwa kuona namna gesi asilia inavyotumika kwenye magari na viwandani.

Wanafunzi hao wametoa wito huo leo tarehe 18 Mei, 2026 wakati wa mkutano wao na  shirika la TPDC waliotembelea majukwaa hayo kukagua maendeleo.

Mwanafunzi  kutoka shule ya sekondari Magamba Loveness Japhet amesema kupitia majukwaa shuleni wanapata elimu kuhusu masuala mbalimbali ya gesi asilia huku akiomba wanafunzi kuwezeshwa kufika kwenye miradi ya utekelezaji wa shughuli za TPDC kujifunza zaidi.

Mwalimu Mlezi wa Jukwaa la wanafunzi sekta ya mafuta na Gesi, shule ya Sekondari ya Wasichana Mkoani Mtwara, Aurelia Kimaro amesema wanafunzi wengi wanashauku ya kutaka kujua namna ambavyo gesi asilia inatumika kwenye magari na viwandani kuzalisha bidhaa mbalimbali.

"Wengi tunavyojua masuala ya gesi asilia ni mapana sana, kuna uchimbaji, utachakataji na pia utumiaji, tunaliomba Shirika la TPDC kuwaandalia wanafunzi ziara kwenye miradi ya utumiaji gesi hiyo kama viwandani na kwenye magari ili wanafunzi wajionee na kujifunza," amesema.

Afisa Maendeleo ya Jamii Mwandamizi  TPDC, Ali Muluge  amesema wanawawezesha wanafunzi ambao wanajiunga na majukwaa ya Mafuta na Gesi kupata elimu kwa kuwapa mahitaji ya kujifunzia na kuwawezesha kufika kwenye miradi mbalimbali ya uchimbaji, na utachakataji.

"Tumepokea ombi la wanafunzi hao kutaka sasa kufika kwenye miradi ambayo inajihusisha na utumiaji wa gesi kama vile viwandani, na tutalifanyia kazi, " amesema.

Amesema TPDC ilianzisha majukwaa ya mafuta na Gesi kwenye shule za sekondari 16 Mikoani Mtwara kwa lengo la kutoa taarifa na elimu sahihi kwa wanafunzi na walimu kuhusu shughuli za serikali kwenye sekta ya mafuta na Gesi.

"Lango lingine la kuanzisha majukwaa haya (Oil and Gas Clubs) ni kuchochea ari ya wanafunzi kupenda kusoma masomo ya Sayansi na kupata wataalamu ambao watalisaidia taifa kutekeleza shughuli kwenye sekta ya mafuta gesi," amesema.











KAMPUNI ya mawasiliano ya simu ya Airtel Tanzania na kampuni ya teknolojia ya Huawei zimethibitisha upya dhamira yao ya kuendelea kuimarisha huduma za mawasiliano nchini kupitia matumizi ya teknolojia za kisasa na ubunifu vilivyojadiliwa katika Kongamano la Huawei Mini Mobile World Congress (Mini MWC).

Kampuni hizo zimesema ushirikiano wao unaendelea kulenga kuharakisha mageuzi ya kidijitali, kupanua huduma za mtandao na kuboresha uzoefu wa wateja kupitia suluhisho za kisasa za mawasiliano.

Akizungumza wakati wa kongamano hilo lililofanyika Tanzania Mei 12, 2026, Mkurugenzi Mtendaji wa Airtel Tanzania, Charles Kamoto, alisema ushirikiano huo unaendelea kuwa sehemu muhimu katika kusaidia ukuaji wa uchumi wa kidijitali nchini.

“Ni furaha kubwa kushiriki nanyi leo tunapojadili mustakabali wa sekta ya mawasiliano, mageuzi ya kidijitali na fursa zinazoendelea kujitokeza ndani ya soko letu na ukanda mzima,” alisema.

Mkutano huo uliwakutanisha viongozi na wataalamu wa kiufundi kutoka kampuni zote mbili kujadili teknolojia za baadaye zinazolenga kuboresha utoaji wa huduma na kuimarisha miundombinu ya mawasiliano nchini Tanzania.

Miongoni mwa maeneo ya kimkakati yaliyojadiliwa ni pamoja na ukuaji wa huduma za intaneti ya simu na majumbani, matumizi ya mitandao msingi inayotumia Akili Unde (AI), maendeleo ya teknolojia ya microwave pamoja na mifumo ya kisasa ya usafirishaji wa taarifa kwa njia ya kidijitali.

Kupitia ushirikiano huo, Airtel Tanzania na Huawei pia walijadili matumizi ya teknolojia za kisasa za wireless na AI zinazolenga kuongeza upatikanaji wa huduma za mtandao, kuboresha uthabiti wa huduma, kuongeza uzoefu wa wateja na kupunguza matumizi ya nishati katika mifumo ya mawasiliano.

Kamoto alisema matumizi ya teknolojia za kizazi kijacho yataongeza matumizi ya data, kusaidia ukuaji endelevu wa biashara na kuiweka Airtel katika nafasi ya kuwa kampuni kinara wa mawasiliano ya kidijitali nchini.

“Tunaendelea kuwa na malengo makubwa na dhamira thabiti katika kusukuma mbele dira ya Airtel kupitia ubunifu na ujumuishaji,” alisema.

Kwa upande wake, Huawei ilisema ushirikiano wake na Airtel Tanzania utaendelea kuwa nguzo muhimu katika safari ya mageuzi ya kidijitali nchini Tanzania.

Kampuni hiyo pia iliipongeza menejimenti ya Airtel Tanzania kwa kushiriki katika majadiliano ya kimkakati yanayolenga kukuza sekta ya mawasiliano nchini na kuhamasisha matumizi ya teknolojia mpya zinazoibukia.

Mini MWC ni jukwaa maalum linaloandaliwa na Huawei Tanzania kwa ajili ya kuwapa wadau fursa ya kujionea teknolojia bunifu zinazooneshwa katika Kongamano la Kimataifa la Mobile World Congress linalofanyika kila mwaka mjini Barcelona, Hispania.

Jukwaa hilo pia linawawezesha wadau wa sekta ya mawasiliano kujadili mwenendo wa teknolojia mpya pamoja na matumizi yanayoongezeka ya Akili Unde (AI) katika kuboresha huduma za mawasiliano nchini.

Baadhi ya viongozi wa Huawei waliohudhuria kongamano hilo ni pamoja na Rais wa Idara ya Bharti Group Key Account, Jack Huang, pamoja na Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa Mauzo wa Huawei Tanzania, Galving Gao.

Kongamano hilo limefanyika wakati ambapo sekta ya mawasiliano nchini Tanzania inaendelea kushuhudia ukuaji mkubwa wa huduma za intaneti, matumizi ya huduma za kidijitali na ongezeko la matumizi ya data kutokana na mahitaji yanayoongezeka ya huduma bora na nafuu za mtandao.
Na Mwandishi Wetu
CHUO Kikuu Kishiriki cha Elimu Dar es Salaam (DUCE) na Wakala wa Elimu Nje ya Nchi Global Education Link (GEL) wamesaini makubaliano ya ushirikiano yatakayolenga kuwatafutia wanafunzi wa chuo hicho fursa mbalimbali za kitaaluma.

Makubaliano hayo yalisainiwa jana jijini Dar es Salaam kati ya Mkurugenzi Mkuu wa GEL, Abdulmalik Mollel, na Kaimu Mkuu wa DUCE, Profesa Pendo Malangwa.

Akizungumza katika hafla hiyo, mgeni rasmi aliyemwakilisha Ofisa Elimu Mkoa wa Dar es Salaam, Geofrey Kituye, aliipongeza GEL na DUCE kwa kuona umuhimu wa kuunganisha nguvu katika kusaidia maendeleo ya elimu na kuwaandaa vijana kwa maisha ya kazi baada ya masomo.

“Nitumie fursa hii kuwapongeza sana DUCE pamoja na Global Education Link kwa kuona umuhimu wa kuunganisha nguvu katika kusaidia maendeleo ya elimu na maandalizi ya vijana wetu kwa maisha ya kazi baada ya hatua mbalimbali za masomo,” alisema Kituye.

Aidha, alisema Dar es Salaam ni mkoa wenye nafasi kubwa katika maendeleo ya taifa kutokana na kuwa na idadi kubwa ya watu, shule za msingi na sekondari za serikali na binafsi, vyuo vya elimu ya juu, hospitali za rufaa na binafsi pamoja na viwanda vikubwa na vya kati vinavyoendelea kukua kila siku.

Alisema ukuaji huo wa uchumi na miundombinu unaongeza wajibu kwa wadau wa elimu kuhakikisha vijana wanapata maarifa, ujuzi, maadili na uwezo wa kutumia fursa zinazozidi kuongezeka ndani ya mkoa huo na taifa kwa ujumla.

“Ndiyo maana suala la kunasihi vijana kuhusu ulimwengu wa kazi baada ya masomo lina umuhimu mkubwa sana katika kipindi hiki. Kimsingi, mwanafunzi wa leo anatakiwa kujitambua mapema, kuelewa uwezo wake, mahitaji yake, ndoto zake na fursa za kazi zilizopo mbele yake,” alisema.

Aliongeza kuwa vijana wanapaswa kusoma wakiwa wanajua wanachosoma, sababu za kusoma taaluma hizo na namna watakavyotumia maarifa na ujuzi wanaoupata katika maisha yao ya baadaye.

Kituye alisema bila mwongozo sahihi wa taaluma, vijana wengi huchagua masomo bila kuzingatia uwezo wao, ndoto zao na mahitaji ya soko la ajira au fursa zinazotarajiwa kujitokeza miaka ijayo.

“Kwa kuzingatia hilo, ni jambo la faraja kuona kuwa DUCE pamoja na Global Education Link wameamua kuunganisha nguvu katika eneo hili muhimu,” alisema.

“Kwa niaba ya Ofisi ya Elimu Mkoa wa Dar es Salaam, napenda kuupongeza tena uongozi wa DUCE pamoja na Global Education Link kwa kuanzisha ushirikiano huu muhimu. Ni imani yangu kuwa hatua hii ni mwanzo wa mabadiliko makubwa katika namna tunavyowaandaa vijana wetu kwa elimu, ajira, ubunifu na maisha ya baadaye,” aliongeza.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Global Education Link, Abdulmalik Mollel, alisema GEL imefikisha miaka 19 katika kazi ya kuwapa wanafunzi mwongozo wa taaluma mbalimbali za kusomea.

Alisema moja ya kazi kubwa zinazofanywa na taasisi hiyo ni kuwatafutia wanafunzi wa Tanzania fursa za kusoma nje ya nchi pamoja na kusaidia kujenga ushirikiano kati ya vyuo vikuu vya ndani na vya nje kwa lengo la kuleta teknolojia na maarifa mapya nchini.

Alisema nchi zilizoendelea zimefikia mafanikio hayo kutokana na uwekezaji mkubwa katika maarifa ya wananchi wake, hivyo GEL imeona umuhimu wa kusaidia kuleta maarifa hayo Tanzania.

Mollel alisema GEL tayari imesaini mikataba ya ushirikiano na vyuo vikuu mbalimbali ikiwemo Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), Mzumbe, Nelson Mandela, TIA na vinginevyo, huku kusaini makubaliano na DUCE ikiwa ni mwendelezo wa juhudi hizo.

“Kila chuo tunachosaini nacho makubaliano tunakuwa na malengo maalum. Leo tumesaini na DUCE kwa ajili ya kutoa mwongozo kwa wanafunzi, na hatuishii kwa wanafunzi pekee; hata wazazi wanaotaka kujiendeleza kielimu au walimu wanaotaka kuongeza elimu tunawapa mwongozo,” alisema Mollel.

Naye Kaimu Mkuu wa DUCE, Profesa Pendo Malangwa, alisema tukio hilo linaonesha dhamira ya dhati ya kuwaandaa vijana katika maisha ya taaluma na ajira za baadaye.

Alisema kupitia ushirikiano huo, wanafunzi wa DUCE watapata mwongozo wa kitaaluma na kufahamu fursa zilizopo ndani na nje ya nchi ili kuwawezesha kukabiliana na ushindani mkubwa wa soko la ajira duniani.

Profesa Malangwa alisema DUCE itaendelea kutekeleza wajibu wake wa kutoa elimu bora, kufanya tafiti na kuandaa wataalamu, huku GEL ikitoa uzoefu wake katika kuwaunganisha vijana na kuwapa ushauri wa maendeleo ya kitaaluma.

Alisema ushirikiano huo unatarajiwa kuongeza mwongozo wa kitaaluma, ushirikishwaji wa wanafunzi, kuwajengea uwezo pamoja na kuimarisha mawasiliano kupitia vyombo vya habari ili kusaidia vijana kuelewa taaluma mbalimbali na mahitaji ya soko la ajira.

“Sote ni mashahidi hapa kwamba vijana wengi wakimaliza kidato cha sita hawana uwezo wa kuchagua wanachotaka kusoma. Wengine wanachagua tu kwa sababu wamesikia kutoka kwa watu wengine. Kupitia ushirikiano huu tunataka vijana wachague taaluma wanazozielewa na zitakazowaletea tija katika maisha yao ya baadaye,” alisema Profesa Malangwa.


-Benki Yathibitisha faida ya Sh bilioni 206 robo ya kwanza 2026.

Na Ashura Mohamed, Arusha

Benki ya CRDB imeahidi kuendelea kulinda misingi bora iliyoiweka katika nafasi nzuri ya kifedha nchini, huku ikichukua hatua za kuongeza kasi ya ukuaji kwa kuunda vitengo maalum vya wataalamu kulenga sekta za kimkakati kama mafuta, gesi, kilimo na madini.

Akizungumza mkoani Arusha wakati wa Mkutano Mkuu wa 31 wa Wanahisa wa benki hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB, Dkt. Abdulmajid Nsekela, alisema lengo ni kuhakikisha benki inatoa huduma zote kwa wakati, kwa urahisi na kwa gharama nafuu, huku ikiendelea kujali mteja.

“Tumeunda vitengo maalum ndani ya benki yetu vyenye wataalamu. Lengo ni kuhakikisha tunafanya vizuri katika sekta hizo na kunasa fursa mpya zitakazojitokeza kwa uwekezaji. Tunachunguza nchi inapoelekea ili tushinde katika maeneo hayo,” alisema Dkt. Nsekela.

Aliongeza kuwa CRDB itaendelea kudumisha mtaji imara, ubora wa mikopo na nidhamu ya kibiashara, huku ikitafuta fursa mpya katika sekta mtambuka kulingana na mwelekeo wa uchumi wa nchi.

Dkt. Nsekela pia aliomba wanahisa kuwa miongoni mwa wateja wa kwanza wa benki yao kwa kutumia huduma mbalimbali za kibenki ili kuiwezesha CRDB kusonga mbele zaidi. Alishukuru Bodi ya Wakurugenzi kwa miongozo na sera ambazo zimekuwa dira ya mafanikio ya benki.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Fedha wa CRDB, Fredrick Nshekanabo, alisema benki imepata faida ya shilingi bilioni 206 baada ya kodi katika robo ya kwanza ya 2026.

Alisema rasilimali za benki zimekua kwa asilimia 35 hadi kufikia shilingi trilioni 23.9, ikilinganishwa na shilingi trilioni 17.6 zilizorekodiwa katika robo ya kwanza ya 2025.

“Ukuaji huu umechangiwa hasa na ukuaji wa mikopo ambao umeongezeka kwa asilimia 34 hadi kufikia shilingi trilioni 14.7. Tunaona ukuaji huo katika mikopo midogo, ya kati na ya kilimo, ambazo ni sekta muhimu kwetu kimkakati,” alisisitiza Nshekanabo.

Aliongeza kuwa Amana pia zimekua kwa asilimia 36 hadi kufikia shilingi trilioni 16.3, jambo linaloonesha kuongezeka kwa imani ya wateja kwa benki.
Mkurugenzi wa fedha wa benki ya CRBB Fredrick Nshekanabo akizungumza wakati wa mkutano mkuu
Mkurugenzi wa benki ya CRBB Dkt.Abdulmajid Nsekela akizungumza na Wanahisa Jijini Arusha

Chama kikuu cha Ushirika Tandahimba Newala Limited (TANECU) kimesema mfumo wa stakabadhi za ghala umeleta mafanikio makubwa kwa wakulima wa korosho pamoja na jamii za Wilaya za Tandahimba na Newala kupitia ongezeko la ushindani wa soko, ajira na ujenzi wa viwanda vya kuongeza thamani ya mazao.

Akizungumza Mei 18, 2026 katika maonesho ya miaka 20 ya mfumo wa stakabadhi za ghala yanayofanyika Jijini Dodoma, Mwenyekiti wa Bodi wa TANECU, Karimu Hamisi Chipola amesema mfumo huo ulianza mwaka 2006 katika Mkoa wa Mtwara hususan kwenye zao la korosho ambapo mwanzoni wakulima hawakuwa na uelewa wa kutosha kuhusu mfumo huo.

Amesema Serikali ilitoa elimu kwa wakulima huku TANECU ikipewa dhamana ya kusimamia mfumo huo kwa wakulima wa zao la korosho katika maeneo yao jambo ambalo limeleta mafanikio makubwa.

Chipola amesema kabla ya kuanzishwa kwa mfumo huo wakulima walikuwa wanauza mazao yao kupitia soko huria bila kuwepo ushindani wala usimamizi mzuri wa bei jambo lililosababisha wakulima wengi kupata hasara.

Amesema baada ya kuanzishwa kwa mfumo wa stakabadhi za ghala, wakulima wamekuwa na uhakika wa soko pamoja na bei nzuri za mazao yao kutokana na ushindani ulioongezeka katika biashara ya korosho.

Aidha amesema mfumo huo umechangia kuongeza ajira katika maeneo yao kupitia shughuli mbalimbali zinazofanyika kwenye maghala ikiwemo watunza maghala, vibarua wa kubeba magunia pamoja na shughuli ndogondogo za biashara zinazofanywa na wananchi.

“Mfumo huu umeleta tija kubwa kwa wakulima na jamii kwa ujumla kwani umeongeza ushindani wa soko na kutoa uhakika wa masoko ya mazao,” amesema Chipola.

Ameongeza kuwa mfumo huo pia umeimarisha vyama vya ushirika ambapo TANECU imeendelea kusimamia ukusanyaji wa tozo mbalimbali za wadau kupitia mfumo huo.

Kwa mujibu wa Chipola, zaidi ya Shilingi Bilioni 6 zimekusanywa na Halmashauri kupitia mfumo wa stakabadhi za ghala jambo lililosaidia kuongeza mapato ya Serikali za Mitaa.

Pia amesema TANECU imefanikiwa kujenga kiwanda cha kubangua korosho chenye thamani ya Shilingi Bilioni 3.6 ambacho kwa sasa kinatoa ajira kwa zaidi ya wananchi 300.

Amesema chama hicho kinaendelea na hatua za mwisho za kujenga kiwanda kingine Wilaya ya Tandahimba kwa lengo la kuongeza thamani ya mazao na kuwapa wakulima ushindani zaidi kwenye soko.

Aidha amesema TANECU kwa sasa ina maghala manne na ipo kwenye mkakati wa kujenga maghala sita zaidi ili kuimarisha uhifadhi wa mazao na kuongeza ufanisi wa mfumo wa stakabadhi za ghala katika maeneo yao.



Jumuiya ya wachimbaji wadogo na wafanyabiashara wa madini ya Metali Tanzania (TBMA) umesema umeanza kuona mafanikio katika kutatua changamoto zinazowakabili wachimbaji wadogo wa madini nchini ikiwemo masoko, viwanda vya uchenjuaji pamoja na kuongeza mapato ya Serikali kupitia sekta ya madini.

Akizungumza Mei 18, 2026 katika Mkutano Mkuu wa Pili wa wanachama wa TBMA uliofanyika Jijini Dodoma, Mwenyekiti wa jumuiya hiyo Thobias Kente amesema wamefanikiwa kuimarisha umoja wa wachimbaji na kuwaunganisha na wenye viwanda vya uchenjuaji wa madini ili kuongeza thamani ya madini.

Kente amesema lengo kuu la jumuiya hiyo ni kuhakikisha utajiri wa madini unawanufaisha wananchi hususan wachimbaji wadogo kwa kuboresha maisha yao kupitia mapato yatokanayo na shughuli za uchimbaji na biashara ya madini.

Amesema kwa sasa wachimbaji wadogo wameanza kupata nafasi kubwa zaidi ya kushiriki katika uchumi wa nchi kupitia sekta ya madini kutokana na juhudi za Serikali na ushirikiano uliopo kati ya wadau wa sekta hiyo.

Kwa upande wake, Katibu wa TBMA, Nobert Kaijage amesema jumuiya hiyo ilisajiliwa mwaka 2024 kwa lengo la kuwa daraja kati ya Serikali na wachimbaji pamoja na kuongeza fursa za uwekezaji na ajira kwa wanachama wake.

Amesema TBMA imeendelea kutoa elimu na ushauri kuhusu uchimbaji salama wa madini huku ikiwa na mpango wa kuwawezesha wachimbaji kupata vifaa vya kisasa kupitia ushirikiano na wadau mbalimbali wa sekta hiyo.

Kaijage amesema mafanikio yaliyopatikana ni pamoja na ongezeko la wanachama hai kutoka 15 hadi 40 pamoja na kuongezeka kwa uelewa wa sheria, kanuni na miongozo ya sekta ya madini kwa wanachama wa jumuiya hiyo.

Aidha amesema mapato ya jumuiya yameongezeka kupitia michango na ada za wanachama huku TBMA ikiendelea kusaidia utatuzi wa changamoto na migogoro ya wachimbaji katika maeneo mbalimbali ikiwemo Kagera, Dodoma na Lindi.

Amesema kupitia jumuiya hiyo wachimbaji wengi wameanza kupata taarifa muhimu kuhusu masoko ya madini, uwekezaji na taratibu za kisheria jambo ambalo limeongeza uelewa na ushiriki wao katika shughuli za madini.

Hata hivyo amesema wachimbaji bado wanakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo ucheleweshaji wa vibali vya mazingira na kemikali kutoka Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali pamoja na mabadiliko ya bei za madini bila taarifa rasmi.

Ameongeza kuwa baadhi ya wanachama wanashindwa kumudu gharama za utafiti wa madini huku baadhi ya viwanda vikishindwa kununua malighafi kwa bei rafiki jambo linaloathiri uzalishaji na biashara ya madini nchini.

Kaijage amesema ucheleweshaji wa majibu ya changamoto kutoka kwa mamlaka husika umekuwa ukiwasababishia hasara wachimbaji wadogo na kupunguza kasi ya maendeleo ya shughuli zao.

Aidha amesema TBMA inaendelea kuiomba Serikali kuweka mazingira bora zaidi yatakayorahisisha upatikanaji wa vibali na kuongeza ushirikiano kati ya wachimbaji na taasisi za Serikali.

Amesema mipango ya jumuiya hiyo ni kuongeza wanachama wapya kupitia ziara, semina na makongamano pamoja na kuwezesha uanzishwaji wa viwanda vya uchenjuaji wa madini ili kuongeza thamani ya madini yanayochimbwa nchini.

Kaijage amesema jumuiya hiyo itaendelea kufanya kazi kwa karibu na Serikali pamoja na wadau wengine wa sekta ya madini ili kuhakikisha wachimbaji wadogo wananufaika zaidi na rasilimali za madini zilizopo nchini.





 


Top News