Na Byera Deus
Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) limeanza kulipa fidia kwa wananchi 280 wa kata nne za Wilaya ya Karagwe wanaopitiwa na mradi wa kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 220 kutoka Benaco hadi Kyaka, kufuatia maagizo yaliyotolewa Mei 9, 2026, na Waziri wa Nishati, Deogratias Ndejembi, wakati wa ziara yake mkoani Kagera.
Mhandisi anayehusika na masuala ya kuchora ramani na kupima ardhi katika mradi huo kutoka Makao Makuu ya TANESCO, Derick Kaijanangoma, alisema jumla ya shilingi bilioni 1.7 zimetolewa kwa ajili ya ulipaji fidia katika awamu ya kwanza kwa wananchi wa kata za Nyaishozi, Nyakahanga, Bugene na Nyakasimbi.
Alisema gharama za mradi za kulipa fidia ni shilingi bilioni 6.1, na Serikali imeanza kutoa fedha kwa wananchi wote wanaopisha ujenzi wa mradi huo katika wilaya za Ngara, Karagwe na Missenyi.
“Zoezi la ulipaji fidia tayari limefanyika katika Wilaya ya Ngara na sasa linaendelea katika maeneo ya Karagwe. Tunajua kwamba tathmini ilifanyika mwaka 2022, lakini sasa muda wa kulipwa fidia umefika, na kila familia itafikiwa. Hata kama muhusika amepoteza maisha, kama nyaraka zimetimia na vigezo vimezingatiwa, atapatiwa haki yake,” alisema Kaijanangoma.
Alisema kuwa baada ya kulipwa fidia, wananchi hawataruhusiwa kuendelea kufanya shughuli zozote za kibinadamu katika maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya mradi, na wametakiwa kuondoa mali zao ndani ya siku 30, huku uwezekano wa kuongezewa muda ukiwepo pale inapobidi ili kumpa nafasi mkandarasi kuendelea na kazi.
Alitoa wito kwa wananchi waliopokea fidia kuhakikisha wanarudisha kilekile kilichofidiwa, kama ni ardhi, nyumba au misitu, na wasitumie fedha hizo katika masuala mengine kama kuongeza mke au kukimbia familia.
Sarafina Gasiliel, Afisa Maendeleo ya Jamii wa mradi huo, alisema changamoto kubwa ambazo wamekutana nazo katika ulipaji wa fidia ni migogoro ya ndoa, migogoro ya ardhi ambayo tayari imethaminishwa pamoja na ukosefu wa elimu ya mirathi.
Alitoa wito kwa wananchi kumaliza migogoro kwanza ili fidia ijulikane inaenda kwa nani, huku wananchi wote waliopoteza ndugu zao waliopaswa kulipwa fidia wakitakiwa kupata msimamizi wa mirathi atakayeweza kupokea fidia hiyo kwa niaba ya wanafamilia wa marehemu.
Kwa upande wao, baadhi ya wananchi akiwemo mkazi wa Kijiji cha Bisheshe, Fidelix Banyesige, wameishukuru Serikali na TANESCO kwa kuanza kulipa fidia licha ya kuchelewa kwake tangu walipofanyiwa tathmini mwaka 2022.
“Tunalishukuru shirika kwa kutulipa fidia. Ingawa imechelewa, tuko tayari kupisha mradi huu kwa manufaa ya wananchi wengine ambao bado hawajapata huduma ya umeme,” alisema Banyesige kwa niaba ya wananchi hao.
Mradi huo wa kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 220 unatarajiwa kuboresha upatikanaji wa huduma ya umeme katika maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Kagera na kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii.



.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)


.jpeg)

.jpeg)


.jpeg)

.jpeg)



.jpeg)


.jpeg)







.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)



.jpeg)