Na Janeth Raphael MichuziTv

Tume ya Uchunguzi wa Matukio ya Uvunjifu wa Amani yaliyotokea wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025, imesema jumla ya watu 518 walipoteza maisha kutokana na ghasia zilizojitokeza siku ya uchaguzi huo.

Akiwasilisha ripoti ya Tume hiyo leo Ikulu jijini Dar es Salaam leo, Mwenyekiti wake Jaji Mkuu Mstaafu Mohamed Othman Chande amesema vifo hivyo vilitokea katika maeneo mbalimbali nchini, huku Mkoa wa Dar es Salaam ukiongoza kwa idadi kubwa zaidi ya wahanga.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo, Dar es Salaam ilirekodi vifo 182, ikifuatiwa na Mwanza (90), Mbeya (80), Arusha (53), na mikoa mingine ikiwa na jumla ya vifo 113.

Jaji Chande amesema kati ya watu 518 waliofariki, wanaume ni 490 sawa na asilimia 94.6, huku wanawake wakiwa 28 (asilimia 5.4). Aidha, alibainisha kuwa sehemu kubwa ya vifo hivyo vilikuwa vya aina isiyo ya kawaida (unnatural deaths).

“Tathmini ya Tume ni kuwa jumla ya vifo vilivyotokana na ghasia za Uchaguzi Mkuu ni 518. Kati ya hivyo, 21 walikuwa watoto,” alisema Jaji Chande.

Kwa mujibu wa takwimu hizo, watoto waliofariki ni pamoja na 15 wenye umri kati ya miaka 15–17, wanne wenye miaka 7–10, na wawili chini ya miaka mitano.

Ripoti hiyo pia imeeleza kuwa vifo 502 (asilimia 96.9) vilikuwa vya raia, huku 16 (asilimia 3.1) wakiwa ni maafisa na askari wa vyombo vya ulinzi na usalama.

Kuhusu mazingira ya vifo hivyo, Tume imesema watu 373 walifikishwa hospitalini wakiwa tayari wamefariki dunia, 121 walifariki wakiwa wanapatiwa matibabu, na miili 24 haikuwa na taarifa kutoka vituo vya huduma za afya.

Aidha, kati ya miili yote 518, miili 480 sawa na asilimia 92.7 ilitambuliwa na kuchukuliwa na ndugu na familia zao.

Ripoti hiyo ni sehemu ya uchunguzi mpana uliofanywa kubaini chanzo na athari za ghasia zilizotokea wakati na baada ya uchaguzi huo.







Benki ya NMB imesema uwekezaji wake katika mifumo ya kidijitali ya ukusanyaji wa mapato umeisaidia Serikali kukusanya zaidi ya Sh trilioni 9.8 kupitia majukwaa yake tangu mwaka 2018.

 Mafanikio hayo yalielezwa Arusha wakati wa mkutano mkuu maalum wa uchaguzi wa viongozi wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT).

Akizungumza katika mkutano huo, Mkurugenzi wa Uhusiano wa Wawekezaji, Uendelevu na Mawasiliano wa NMB, Innocent Yonazi, alisema hatua hiyo imetokana na ushirikiano wa karibu kati ya benki hiyo na taasisi za umma katika kuboresha usimamizi wa mapato ya Serikali. 

Alisema NMB imewekeza katika mifumo ya kisasa ya malipo inayorahisisha malipo ya Serikali kwa wananchi, wafanyabiashara na taasisi mbalimbali kwa uwazi, urahisi na ufanisi mkubwa, huku ikisaidia kupunguza mianya ya upotevu wa mapato.

Yonazi alisema pia benki hiyo imeendelea kupanua wigo wa ujumuishaji wa kifedha nchini kwa kufikia zaidi ya vijiji 3,000 na kufungua zaidi ya akaunti milioni mbili mpya. Aliongeza kuwa thamani ya mali za NMB imeongezeka kutoka Sh trilioni 7.1 mwaka 2020 hadi Sh trilioni 17.2 mwaka 2025, sawa na ongezeko la asilimia 142, huku faida kabla ya kodi ikifikia Sh trilioni 1.1.

Akifungua mkutano huo Aprili 22, 2026, Waziri Mkuu Dk. Mwigulu Lameck Nchemba aliwataka viongozi wa serikali za mitaa kuikuza sekta binafsi ili ichochee zaidi ukuaji wa uchumi na kusaidia kufikiwa kwa Dira ya Taifa ya 2050 ya uchumi wa dola trilioni 1. 

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa ALAT, Murshid Ngeze, alisema mkutano huo umewakutanisha zaidi ya wajumbe 400 kwa ajili ya kuchagua viongozi wapya watakaoiongoza jumuiya hiyo kwa kipindi cha miaka mitano ijayo.

Mkurugenzi wa Uhusiano wa Wawekezaji, Uendelevu na Mawasiliano wa Benki ya NMB, Innocent Yonazi, akizungumzia mafanikio ya taasisi hiyo mbele ya Waziri Mkuu Dr Mwigulu Nchemba katika mkutano mkuu maalum wa uchaguzi wa viongozi wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT) unaofanyika Arusha.
Meneja kanda ya kati wa Benki ya NMB Janeth Shango akiteta jambo na Makamu Mwenyekiti wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT) Sima Constantine Sima katika mkutano mkuu maalum wa uchaguzi wa viongozi wa unaofanyika Arusha.Kulia ni Josephine Kulwa Meneja  Mwandamizi wa biashara za serikali.


-Asema kuna miradi inakwama utekelezaji sababu ya migawanyiko

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amewataka viongozi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa waepuke migogoro na mizozo kwa sababu kuna miradi inakwama utekelezaji kutokana na migawanyiko.

“Twendeni tukatimize wajibu wetu, tuache migawanyiko kwa sababu hayo si matarajio ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan,” amesisitiza wakati akizungumza na washiriki wa Mkutano Mkuu Maalum wa Uchaguzi wa Viongozi wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT) katika ukumbi wa mikutano wa AICC, jijini Arusha.

Ametoa wito huo leo jioni (Jumatano, Aprili 22, 2026) wakati akifungua mkutano huo wa siku mbili ulioanza leo na kusisitiza kuwa waangalie uwezekano wa kuondoa uchaguzi wa Makamu Mwenyekiti ambao hivi sasa unafanyika kila mwaka.

“Tuepuke migogoro, Waheshimiwa Mameya, Madiwani na Wenyeviti; kuna baadhi ya maeneo tunachelewa kutekeleza miradi ya maendeleo kwa sababu ya migogoro inayotengeneza migawanyiko.”

“Ondoeni utaratibu wa kuchagua Makamu Mweneyekiti kila mwaka kwani jambo hili linaleta makovu. Nimeshamuagiza Waziri wa TAMISEMI amuandikie Mwanasheria Mkuu wa Serikali kama ni sheria ifutwe, kama ni kanuni ibadilishwe, lakini kama mkutano huu una mamlaka, utaratibu wa kuchagua Makamu Mwenyekiti kila mwaka ufutwe,” amesisitiza.

Waziri Mkuu amesema utaratibu wa sasa unawanyima fursa viongozi walioko madarakani kujielekeza kwenye masuala ya kuwaletea maendeleo wananchi na badala yake wanajikuta kwenye harakati za kugawana vyeo.

“Wenyeviti wanajikuta wanaongoza watu waliogawanyika na hili halileti tija. Hivi sasa walioko madarakani bado wanajifunza kazi, tayari wengine wameshaanza kampeni kuwania nafasi zao,” amesisitiza.

Aidha, aliwataka viongozi watakaochaguliwa kesho wahakikishe wanakuwa chachu ya maendeleo na kusimamia maslahi ya wananchi kwa vitendo na kuongeza: “Kwa viongozi mtakaochaguliwa, mhakikishe mnakwenda kusaidia Jumuiya yetu na maslahi ya wananchi, muwe viongozi wanaopinga rushwa kwa vitendo. Mhakikishe mnakuwa daraja la kuleta maendeleo kwa wananchi na kuitafsiri Dira ya 2050.”

Wakati huohuo, Waziri Mkuu amesema sekta binafsi ina nafasi kubwa katika kufanikisha Dira ya Taifa 2050, akiwataka viongozi wa Halmashauri wawe wasimamizi na walezi wa mazingira rafiki ya uwekezaji.

“Katika DIRA 20250, sekta binafsi imepewa asilimia 70 za kutoa mchango. Wakurugenzi na Wenyeviti wa Halmashauri mkawe walezi wa sekta binafsi. Mkitanguliza kulea sekta binafsi mtakuza mapato. Mkitanguliza mapato mtaua sekta binafsi. Sekta binafsi tunaitegemea sana katika kutengeneza ajira kwa akinamama na vijana,” alisisitiza.

Aidha, aliwataka viongozi hao kutojihisi dhaifu katika utekelezaji wa majukumu yao, akisisitiza kuwa Serikali inatambua mchango wao mkubwa licha ya changamoto chache zinazojitokeza.

“Msipate unyonge, Mheshimiwa Rais anatambua kazi kubwa ya usimamizi wa miradi ya maendeleo mnayoifanya; ni kweli kuna baadhi ya wachache wanaotuangusha, lakini wengi wenu mnafanya kazi vizuri sana,” alisisitiza.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu aliwahakikishia wajumbe wa mkutano kuwa Serikali inaendelea kulifanyia kazi suala la kuboresha maslahi ya madiwani kama ambavyo liliwasilishwa na Mwenyekiti wa ALAT anayemaliza muda wake, Bw. Murshid Ngeze.

“Niwahakikishie Mheshimiwa Rais anatambua kazi kubwa madiwani mnayoifanya; jambo lenu linajitosheleza na linaeleweka, Serikali inaendelea kulifanyia kazi,” amesema.







Josephine Majura, WF, Dodoma


Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), amesema kuwa Serikali inatekeleza mkakati wa Mfumo wa Kodi ya Makadirio (Presumptive Tax Scheme) ili kuwahamasisha walipakodi wadogo wasiokuwa na kumbukumbu sahihi za mapato kusajili biashara zao na kuanza kulipa kodi kwa hiari.

Ameyasema hayo bungeni jijini Dodoma, wakati akijibu swali la Mbunge wa Busokelo Mhe. Lutengano Mwalwiba, aliyetaka kujua mpango wa Serikali wa kuweka vivutio maalum vya kikodi kwa Vijana wanaoanza biashara ili kuchochea ajira na kukuza uchumi.

Mhandisi Munde, alisema kuwa, mkakati huo unaolenga kuwasaidia walipakodi wadogo wasiokuwa na kumbukumbu sahihi za mapato au vitabu vya hesabu, kwa kuwa masharti yake ni mepesi na yanatabirika.

“Serikali pia imeanzisha utaratibu wa kipindi cha neema (grace period) kinachowaruhusu wafanyabiashara wapya kufanya biashara bila kulipa kodi kwa muda wa miezi sita tangu kuanza shughuli zao ili kutoa nafasi kwa wajasiriamali kukuza biashara zao na kujiimarisha kabla ya kuanza kulipa kodi”, alisema Mhandisi Munde.

Alisema kuwa Serikali inatambua umuhimu wa kutoa vivutio maalum vya kikodi kwa vijana ili kuchochea uanzishaji wa biashara na ajira, ikiwemo msamaha wa kodi na viwango pungufu, huku ikiendelea kufanya tathmini ya athari zake ili kuhakikisha usawa, ufanisi wa sera, na uendelevu wa mapato ya Serikali.

Kupitia Sheria ya Fedha ya Mwaka 2023 na Maboresho ya Mwaka 2024, Serikali pia imetoa ahirisho la kodi ya mapato (Corporate Income Tax) kwa kipindi cha miezi sita ya mwanzo kwa biashara mpya (start-ups), hatua inayolenga kusaidia biashara changa kukua na hatimaye kuwa na walipakodi wakubwa na endelevu.



Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania(TCAA), kama sehemu ya kurudisha kwa jamii, imetoa msaada katika kituo cha kulelea watoto cha Tupendane kilichopo jijini Dodoma huku ikitoa wito kwa wadau mbalimbali kuendelea kuwa na moyo wa kusaidia jamii, hususan vituo vya kulelea watoto.

Akizungumza wakati wa kupokea msaada huo, Subira Yasini, mlezi wa Kituo cha Tupendane, ameishukuru TCAA kwa kuguswa na mahitaji ya kituo hicho na kueleza kuwa msaada huo utasaidia kuboresha huduma na mazingira ya malezi kwa watoto waliopo kituoni. Alisema hatua hiyo inaonesha mshikamano na kujali ustawi wa makundi yenye uhitaji maalum katika jamii.

Awali, Bi. Subira alieleza changamoto mbalimbali zinazowakabili, ikiwa ni pamoja na ukosefu wa eneo la kudumu la makazi ya watoto hao, kwani kwa sasa wanatumia eneo la mtu aliyewapatia hifadhi ya muda.

Kituo hicho cha Tupendane kina jumla ya watoto 35, ambapo 22 kati yao wanasoma katika ngazi mbalimbali kuanzia elimu ya msingi hadi sekondari.

Kwa upande wake, Ally Changwila, Meneja Uhusiano wa Mamlaka hiyo kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa TCAA Bw. Salim Msangi, alisema kuwa Mamlaka hiyo inaendelea kuimarisha mahusiano chanya na jamii kwa kushiriki katika shughuli za maendeleo ya kijamii. Ameeleza kuwa msaada uliotolewa katika kituo hicho unaakisi dhamira ya TCAA ya kuchangia ustawi wa jamii sambamba na majukumu yake ya msingi katika usimamizi wa usafiri wa anga.

Aidha, aliongeza kuwa Mkurugenzi Mkuu wa TCAA ameelekeza kuwa, kutokana na umuhimu wa kurejesha kwa jamii na kusaidia wenye uhitaji, kila robo ya mwaka wa fedha angalau TCAA itoe msaada katika mojawapo ya vituo vyake vya kazi nchini. TCAA ina vituo 16 nchi nzima vinavyotoa huduma ya uongozaji ndege.

Kwa upande wake, Aswile Kamendu, Meneja wa TCAA Kituo cha Dodoma, alisema kuwa TCAA itaendelea kushirikiana na Taasisi na vituo mbalimbali vya kijamii katika mkoa wa Dodoma na mikoa mingine ili kusaidia juhudi za Serikali na wadau wengine katika kuboresha maisha ya wananchi.

Msaada uliotolewa katika kituo hicho cha Tupendane ni pamoja na vyakula vya aina mbalimbali, sabuni, mafuta ya kupikia pamoja na vifaa vya shule ikiwemo mabegi na madaftari.
Meneja Uhusiano wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania(TCAA) Ally Changwila (wa pili kulia) aliyemwakilisha Mkurugenzi Mkuu wa TCAA Bw. Salim Msangi pamoja na  Meneja wa TCAA Kituo cha Dodoma Aswile Kamendu wakiwa kwenye picha ya pamoja na baadhi ya walezi na watoto wanaolelewa katika  kituo cha Tupendane kilichopo jijini Dodoma
Meneja Uhusiano wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania(TCAA) Ally Changwila akitoa salamu za Mkurugenzi Mkuu wa TCAA Bw. Salim Msangi wakati wa kutoa msaada katika kituo cha kulelea watoto cha Tupendane kilichopo jijini Dodoma
Meneja wa TCAA Kituo cha Dodoma Aswile Kamendu akizungumza kuhusu namna watakavyoendelea kushirikiana na Taasisi na vituo mbalimbali vya kijamii kwa kutoa misaada mbalimbali katika mkoa wa Dodoma  


Farida Mangube Sikonge, Tabora

Mkuu wa Wilaya ya Sikonge Thomas Mnyinga amewataka wakazi wa wilaya hiyo kulinda na kuhifadhi misitu ya miombo, akieleza kuwa rasilimali hiyo imeanza kuwa kivutio muhimu cha utalii na inaweza kuchangia ukuaji wa uchumi wa eneo hilo.

Akizungumza katika Tamasha la Staff Tour 2026 lililofanyika ndani ya hifadhi ya msitu wa mazingira Itulu hills na kubebwa na kauli mbiu “Tunaungana, Tunaitunza, Tunaburudika na Miombo,” Mkuu huyo wa Wilaya alisema ni muhimu kwa jamii kubadili mtazamo na kuitunza misitu hiyo kwa manufaa ya sasa na vizazi vijavyo.

Alisema pamoja na umuhimu wa miombo, bado kuna matumizi makubwa ya miti hiyo, hususan katika ukaushaji wa tumbaku ambapo wakulima hutumia kuni kwa wingi.

“Serikali ipo katika mpango wa kuleta mbadala wa kukaushia tumbaku ili kupunguza matumizi ya kuni na kulinda misitu yetu,” alisema.

Aliongeza kuwa uhifadhi wa misitu hiyo utasaidia kukuza utalii wa mazingira, ambao unaanza kujitokeza katika maeneo mbalimbali ya wilaya hiyo.

Miongoni mwa vivutio vilivyotajwa ni Mto Koga, ambao unatenganisha mikoa ya Tabora na Katavi. Mto huo umeelezwa kuwa na uhai wa viumbe mbalimbali wakiwemo viboko wanaoonekana katika baadhi ya maeneo.

Aidha, ndege wa aina mbalimbali huonekana katika eneo la mto huo wakifika kutafuta chakula, hali inayoongeza mvuto kwa watalii wanaopenda kutazama wanyamapori na ndege.

Akizungumzia tamasha hilo, Afisa Utalii kutoka Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) Wilaya ya Sikonge Mhifadhi John Shayo alisema lengo ni kuhamasisha utalii wa miombo na kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa uhifadhi wa misitu hiyo yenye bioanuai kubwa.

“Tunataka jamii itambue kuwa misitu hii ina thamani zaidi ya matumizi ya kawaida, ikiwemo fursa za utalii,” alisema.

Mbali na shughuli za utalii wa asili, washiriki wa tamasha hilo pia walipata fursa ya kufurahia burudani mbalimbali zikiwemo ngoma za asili pamoja na vyakula mbalimbali ikiwemo nyama choma.

Tamasha hilo limeelezwa kuwa sehemu ya jitihada za kukuza utalii wa ndani huku likihamasisha uhifadhi wa rasilimali misitu katika Wilaya ya Sikonge.














Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma

Waziri wa Nishati, Deogratius Ndejembi, amewasilisha bungeni mjini Dodoma makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Nishati kwa mwaka wa fedha 2026/2027, akieleza kuwa jumla ya Shilingi trilioni 2.525 zimetengwa kwa ajili ya utekelezaji wa majukumu ya wizara hiyo.

Akiwasilisha bajeti hiyo, Waziri Ndejembi amesema kati ya fedha hizo, Shilingi trilioni 2.462 sawa na asilimia 97.5 ya bajeti yote ni kwa ajili ya matumizi ya maendeleo. Kati ya fedha za maendeleo, Shilingi trilioni 1.602 ni fedha za ndani, huku Shilingi bilioni 859.9 zikiwa ni fedha kutoka nje ya nchi kwa ajili ya kugharamia miradi mbalimbali ya kimkakati katika sekta ya nishati.

Aidha, amesema jumla ya Shilingi bilioni 63.036 zimetengwa kwa ajili ya matumizi ya kawaida, sawa na asilimia 2.5 ya bajeti yote ya wizara. Kati ya fedha hizo, Shilingi bilioni 52.939 zimetengwa kwa ajili ya mishahara ya watumishi (PE), wakati Shilingi bilioni 10.097 zikitengwa kwa matumizi mengineyo ya kawaida (OC) kwa Wizara ya Nishati na taasisi zake, ikiwemo PURA.

Waziri Ndejembi alisisitiza kuwa bajeti hiyo inalenga kuimarisha upatikanaji wa nishati ya uhakika, kuendeleza miradi ya kimkakati na kuchochea ukuaji wa uchumi wa taifa kupitia sekta ya nishati.


 

  

Meneja wa Ufungaji wa Mgodi wa Barrick Buzwagi, Mhandisi Zonnastral Mumbi, akizungumza katika Mahafali ya 14 ya Kidato cha Sita ya Shule ya Sekondari Mwendakulima, Manispaa ya Kahama, mkoani Shinyanga.
Meneja wa Ufungaji wa Mgodi wa Barrick Buzwagi, Mhandisi Zonnastral Mumbi, akizungumza katika Mahafali ya 14 ya Kidato cha Sita ya Shule ya Sekondari Mwendakulima, Manispaa ya Kahama, mkoani Shinyanga.
Meneja wa Ufungaji wa Mgodi wa Barrick Buzwagi, Mhandisi Zonnastral Mumbi, akizungumza katika Mahafali ya 14 ya Kidato cha Sita ya Shule ya Sekondari Mwendakulima, Manispaa ya Kahama, mkoani Shinyanga.

Naibu Meya wa Manispaa ya Kahama na Diwani wa Kata ya Mwendakulima, Shabani Mikongoti, akizungumza katika Mahafali ya 14 ya Kidato cha Sita ya Shule ya Sekondari Mwendakulima, Manispaa ya Kahama, mkoani Shinyanga.
Naibu Meya wa Manispaa ya Kahama na Diwani wa Kata ya Mwendakulima, Shabani Mikongoti, akizungumza katika Mahafali ya 14 ya Kidato cha Sita ya Shule ya Sekondari Mwendakulima, Manispaa ya Kahama, mkoani Shinyanga.
Mkuu wa Shule ya Sekondari Mwendakulima, Bi. Neema Mfumya, akizungumza katika Mahafali ya 14 ya Kidato cha Sita ya Shule ya Sekondari Mwendakulima, yaliyofanyika Manispaa ya Kahama, mkoani Shinyanga.
Mkuu wa Shule ya Sekondari Mwendakulima, Bi. Neema Mfumya, akizungumza katika Mahafali ya 14 ya Kidato cha Sita ya Shule ya Sekondari Mwendakulima, yaliyofanyika Manispaa ya Kahama, mkoani Shinyanga.
Agnes Julius akisoma risala kwa niaba ya wahitimu katika Mahafali ya 14 ya Kidato cha Sita ya Shule ya Sekondari Mwendakulima, Manispaa ya Kahama, mkoani Shinyanga.
Meneja wa Ufungaji wa Mgodi wa Barrick Buzwagi, Mhandisi Zonnastral Mumbi, akigawa vyeti kwa wahitimu katika Mahafali ya 14 ya Kidato cha Sita ya Shule ya Sekondari Mwendakulima, yaliyofanyika Manispaa ya Kahama, mkoani Shinyanga.
Meneja wa Ufungaji wa Mgodi wa Barrick Buzwagi, Mhandisi Zonnastral Mumbi, akiwa katika Mahafali ya 14 ya Kidato cha Sita ya Shule ya Sekondari Mwendakulima, yaliyofanyika Manispaa ya Kahama, mkoani Shinyanga.
Meneja wa Ufungaji wa Mgodi wa Barrick Buzwagi, Mhandisi Zonnastral Mumbi, akigawa vyeti kwa wahitimu katika Mahafali ya 14 ya Kidato cha Sita ya Shule ya Sekondari Mwendakulima, yaliyofanyika Manispaa ya Kahama, mkoani Shinyanga.
Wahitimu wakiwa katika Mahafali ya 14 ya Kidato cha Sita ya Shule ya Sekondari Mwendakulima, Manispaa ya Kahama, mkoani Shinyanga.

*

Kampuni ya Barrick nchini yenye ubia na Serikali ya Tanzania kupitia kampuni ya Twiga Minerals imeeleza dhamira yake ya kuendelea kuunga mkono jitihada za Serikali katika kuhakikisha wanafunzi wanapata elimu bora katika mazingira salama na rafiki kwa kujifunzia.

Top News