Na Seif Mangwangi, Michuzi TV Arusha

SERIKALI imesema Mwitikio wa vijana kutaka kukopeshwa fedha kwaaji li ya kuanzisha biashara umekuwa mkubwa na wa kutia moyo baada ya baadhi ya masharti magumu yaliyokuwa yakiwashinda vijana kuondolewa.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa programu ya Kitaifa ya utoaji wa mikopo kupitia programu ya billioi 200 chini ya mfuko wa maendeleo ya vijana leo 9 Julai 2026,Jijini Arusha, Waziri wa nchi ofisi ya Rais Vijana, Joel Nananuka amesema miongoni mwa changamoto zilizokuwa zikilalamikiwa ni riba kubwa kwa wakopaji.

“Riba ilikuwa ni changamoto, na Sasa riba imeondolewa mtu akishapata mikopo na kulipa bima basi atapata mikopo wake, pia kulikuwa na changamoto ya mikopo kurejesha mapema, tunataka mtu akipata fedha aanze kufanyia kazi ndipo aanze kurejesha, mwongozo mpya ni kwamba watakaa na mkopo kwa miezi mitatu kabla ya kuanza kurejesha,” amesema.

Amesema changamoto nyingine iliyofanyiwa mabadiliko ni mtu mmoja mmoja kupata fedha kama alivyoomba badala ya kuwa katika kikundi ndio update fedha hizo kama ilivyokuwa hapo awali.

“ Ilikuwa fedha zinatolewa kwa vikundu pekee na sio mtu mmoja mmoja lakini sasa hivi kama tulivyoagizwa na Mheshimiwa Rais Samia tuondoe vikwazo vyote, basi awamu hii vijana wengi watapata mkopo Kwa namna alivyoomba bila kupitia kikundi,” amesema.

Amesema baada ya kutatuliwa Kwa changamoto hizo, jumla ya maombi 30,384 yalipokelewa kutoka maeneo mbalimbali nchini yakihusisha sekta za kilimo, mifugo, uvuvi, viwanda vidogo, biashara, ubunifu, teknolojia na huduma mbalimbali.

“ Takwimu hizi zinaonesha wazi kuwa vijana wa Tanzania si wavivu kama ambavyo wakati mwingine imekuwa ikidaiwa;

badala yake, wanahitaji mazingira yanayowapa fursa ya kuonesha uwezo wao,” amesema Nanauka na kuongeza:

“Baada ya mchakato wa kina wa tathmini uliozingatia vigezo vilivyowekwa, kwa awamu ya kwanza tunaenda kuwezesha miradi ya vijana yenye thamani ya Shilingi Bilioni 8 kupitia Mfuko wa Maendeleo ya vijana unapojaribiwa na Ofisi ya Rais - Maendeleo ya vijana,” amesema.

Amesema katika uzinduzi wa programu hiyo, katika Mkoa wa Arusha mikopo ya shilingi milioni 730 itatolewa ambapo milioni 500 zitaenda katika utafiti na utengenezaji wa dawa za binadamu, Milioni 130 zitaenda katika kiwanda cha vijana kinachotengeneza chaki zisizotoa vumbi na milioni 100 zitaenda kwa viundi vya Mama na Baba Lishe.

“ Hii ni hatua ya mwanzo ambayo itaendelea kupanuliwa kadri fedha zitakavyopatikana na tathmini za utekelezaji zitakavyoendelea kuonesha mafanikio,” amesema.

Amesema fedha hizo ni za uwekezaji wa Taifa kwa vijana wake na kwamba Serikali imewaamini na imeamua kuwekeza kwa vijana kwa matarajio kwamba watazitumia kuongeza uzalishaji, kupanua biashara, kuanzisha viwanda vidogo, kuongeza thamani ya bidhaa na kuzalisha ajira kwa vijana wengine.

“Napenda kuwasisitiza kuwa mafanikio ya programu hii hayatapimwa kwa kiwango cha fedha kilichotolewa, bali kwa matokeo yatakayopatikana. Tunataka kuona biashara zenye tija, ongezeko la mapato ya kaya, ajira mpya, ukuaji wa kampuni za vijana na mchango mkubwa wa sekta ya vijana katika pato la Taifa, “ amesema na kuongeza:

“Hivyo basi, nawasihi mtumie fedha hizi kwa malengo yaliyokusudiwa; wekeni mifumo mizuri ya usimamizi wa fedha; tunzeni kumbukumbu za biashara zenu; zingatieni misingi ya utawala bora wa biashara; na hakikisheni mnarejesha mikopo kwa wakati. Nidhamu ya fedha ndiyo msingi wa mafanikio ya biashara yoyote duniani.” Amesema.

Awali Mkuu wa Mkoa wa Arusha CPA Amos Makala amesema vijana wa Arusha wanajitambua na hawachezi na fursa na kwamba Kwa juhudi wanazoendelea nazo ana uhakika kesho yao itakuwa njema.

Mwakilishi wa benki ya CRDB, Meneja wa Benki hiyo tawi la Meru Arusha, Haika Mawalla amesema CRDB Bank inajivunia kuaminiwa na Serikali kupewa jukumu la kusimamia utekelezaji wa mpango huo wa uwezeshaji wa vijana nchini kote.

“ Hili ni jukumu kubwa na tunalipokea kwa uzito, uadilifu na uwajibikaji. Tumejipanga kuhakikisha huduma hii inawafikia vijana wengi iwezekanavyo kwa uwazi, ufanisi na weledi,” amesema.

Amesema mbali na kutoa mikopo, CRDB itaendelea kuwajengea vijana uwezo kupitia elimu ya fedha, usimamizi wa biashara na matumizi sahihi ya mikopo na kwamba wanaamini kuwa mchanganyiko wa mtaji, maarifa na nidhamu ya fedha ndio msingi wa mafanikio ya biashara na ujasiriamali endelevu.

“Tunawasihi vijana wote kuitumia fursa hii kwa ubunifu, uwajibikaji na uaminifu. Mikopo hii ni chachu ya maendeleo; itumike kuanzisha na kukuza miradi yenye tija, kuongeza ajira na kuinua uchumi wa familia na Taifa kwa ujumla,” amesema.






Na Janeth Raphael MichuziTv

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema Watanzania wanahitaji amani, usalama na utulivu badala ya vurugu na mivutano ya kisiasa, akisisitiza kuwa mazingira hayo ndiyo msingi wa Serikali kuendelea kutoa huduma bora za kijamii, kukuza uchumi na kuongeza fursa za ajira kwa wananchi.

Rais Samia ametoa kauli hiyo leo Alhamisi, Julai 9, 2026, visiwani Zanzibar wakati wa hafla ya kushuhudia utiaji saini wa Tamko la Pamoja la Maridhiano ya Kisiasa kati ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na ACT Wazalendo.

Amesema maridhiano ya kisiasa hayapaswi kutafsiriwa kama ishara ya udhaifu, bali ni alama ya ukomavu wa kisiasa unaojenga msingi wa umoja, kuheshimiana na ushirikiano miongoni mwa viongozi wenye mitazamo tofauti kwa maslahi ya taifa na wananchi.

Kwa mujibu wa Rais Samia, hatua hiyo inafungua ukurasa mpya wa kuimarisha mshikamano, amani na utulivu nchini, hususan Zanzibar, huku akihimiza siasa kujengwa katika misingi ya hoja, heshima na ustaarabu badala ya chuki, migawanyiko na mivutano isiyo na tija.

Amesema migogoro na siasa za chuki huzuia maendeleo, lakini maridhiano na siasa za staha huweka mazingira bora ya utekelezaji wa mipango ya maendeleo na kuboresha ustawi wa wananchi.

Rais Samia pia amezitaka pande zote zinazohusika na maridhiano hayo kuheshimu makubaliano yaliyofikiwa, kuendelea na mazungumzo kwa uwazi na kujenga imani ili kulinda umoja, amani na usalama wa taifa.

Akihitimisha hotuba yake, Rais Samia amesisitiza umuhimu wa kudumisha mshikamano uliojengwa kupitia maridhiano hayo.

"Hekima tuliyoionesha leo ikalindwe kwa matendo mema ya kesho, na imani tuliyoijenga kwa muda mrefu isiangushwe kwa maneno au mienendo isiyo na tija," amesema Rais Samia.

















JESHI la Polisi Mkoa wa Kilimanjaro linamshikilia mtu mmoja aitwaye Beatrice Urassa (59) kwa tuhuma za mauaji ya watu wanne ambao walifariki dunia kwa nyakati tofauti wakiwa wanapatiwa matibabu katika hospitali ya Machame Wilayani Hai.

Akithibitisha kukamatwa kwake, Kamanda wa Polisi mkoa wa Kilimanjaro, SACP Saimon Maigwa aliwataja waliofariki dunia ni Hamida Hamis Kweka (26), Robson Edson Meena (34), Ismail Exaud Uronu (34) na Kamama Exaud Uronu (45) wote wakazi wa kitongoji cha kinyaro, kata ya Mnadani, wilaya ya Hai na Mkoa wa Kilimanjaro.

Kamanda Maigwa alisema kuwa, uchunguzi wa awali umebaini kuwa, mtuhumiwa huyo anadaiwa kuwapatia dawa za kienyeji watu hao ambao ni ndugu wa familia moja, na kupelekea kufariki dunia wakiwa wanapatiwa matibabu Julai 05 mwaka huu majira ya usiku.

Jeshi la Polisi Mkoa wa Kilimanjaro linaendelea na uchunguzi kuhusina na tukio hili, pindi utakapokamilika taratibu nyingine za kisheria zitafuata.


ZAIDI ya Bilioni saba (7) zimekamilisha ujenzi wa soko la kimataifa la mazao katika kijiji cha Kanondo halmashauri ya Manispaa ya Sumbawanga mkoani Rukwa.

Akizungumza wakati akikagua eneo la soko la kimataifa la mazao Waziri wa katiba na sheria Juma Homera ameitaka halmashauri ya Manispaa ya Sumbawanga kuanza kutumia soko hilo ifikapo August mosi mwaka huu.

Amewapongeza halmashauri kwa kusimamia na kukamilisha mradi huo huku akiwasisitiza kuendelea kusimamia miradi ya maendeleo kwa uwazi na uadilifu.

Aidha mstahiki meya wa Halmashauri ya Manispaa ya Sumbawanga Frenk Lupimo ameeleza umuhimu wa soko hilo kuwa linauwezo wa kuchukua tani 19,000 na litasaidia kukuza mapato ya ndani na kukuza uchumi kwa wafanyabiashara watakao tumia soko hilo.

Kwa upande wao wananchi wa eneo hilo wamemshukuru Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa ujenzi wa soko la mazao na kuwa soko hilo linakwenda kutatua changamoto na kuondoa walanguzi waliokuwa wakiwaibia wakulima.

Pia wameeleza kuwa awali walikuwa wakiibiwa na walanguzi kutoka nchi jirani wakitumia vipimo vinavyo waumiza wakulima ambapo kwa kujengwa kwa soko hilo tatizo hilo linakwenda kumalizika kwasababu wakulima na wafanyabiasha watauza na kununua mazao katika soko hilo.




Jane Mwakyoma - Rukwa.

WAKAZI wa kata ya Msua Manispaa ya Sumbawanga mkoani Rukwa wameishukuru serikali ya awamu ya sita kwa ujenzi wa shule ya msingi Kisiwani inayowasaidia wanafunzi wa eneo hilo kupata elimu karibu na makazi yao.  

Wakizungumza baada ya waziri wa katiba na sheria Juma Homera kutembelea na kukagua ujenzi unaoendelea shuleni hapo wananchi wamesema ujenzi wa shule hiyo unasaidia watoto kupata elimu karibu na makazi yao ukilinganisha na hapo awali walikuwa wakifuata elimu hiyo zaidi ya km 3 hali iliyokuwa ikihatarisha usalama wa watoto hao.

Akimwakilisha mwalim mkuu wa shule ya msingi Kisiwani Efrahim Kimario amesema walipokea fedha za ujenzi zaidi ya Milioni 329 ikiwa majengo sita yamekamilika na tayari yanatumika huku jengo la utawala likiwa katika hatua ya umaliziaji kuhakikisha watoto wa eneo hilo wanaendelea kupata elimu ya msingi shuleni hapo.

Aidha amesema ujenzi wa shule hiyo unatumia mfumo wa Force Account ambapo alimshukuru Mbunge wa jimbo la Sumbawanga mjini Aishi Khalfan Hilali na Dtk. Samia Suluhu Hassan kwa jitihada walizofanya kuhakikisha shule inajengwa na watoto wanapata elimu ya uhakika.

Kwa upande wake Waziri wa katiba na sheria Juma Homera amepongeza halmashauri ya Manispaa ya Sumbawanga kwa usimamizi wa mradi na kuhakikisha baadhi ya majengo yanakamilika na kuendelea kutoa huduma kwa wanafunzi.

Pia Homera amewataka viongozi wa serikali nchini kusimamia kikamilifu miradi ya maendeleo na kuhakikisha inakamilika kwa wakati ili kuepusha migogoro ya wananchi na serikali.



Tukio la Ngorongoro kuonesha vivutio vya utalii mubashara kupitia runings kubwa iliyofungwa katika banda la Wizara ya Maliasili na Utalii

limevutia wananchi wengi wanaotembelea  maonesho ya 50 ya biashara ya kimataifa jijini  Dar es Salaam kwa kuoneshwa maajabu yaliyopo Ngorongoro hususan Kreta ya Ngorongoro, makundi ya wanyama mbalimbali ikijumuisha pundamilia, nyumbu, swala, nyati na wanyama adimu kama  faru, simba, tembo na  na  chui na kujihisi kama wapo nyumbani Ngorongoro.

Afisa Uhusiano Mkuu wa Ngorongoro Bw. Walter Mairo ameeleza kuwa  kupitia runinga iliyofungwa viwanja vya maonesho wageni wanaotembelea wanaona wanyama aina mbalimbali ndani ya Kreta, tambarare za Ndutu ambapo maisha ya Nyumbu kuzaliwa, kukua, kusafiri na kurejea na kuanza kizazi kipya kila mwaka

Mairo ameongeza kuwa, matukio mubashara yanaonesha wananchi jinsi teknolojia ya kidigitali na utalii wa asili vinavyoweza kushirikiana kuelimisha, kuburudisha na kuonyesha ushahidi kuwa Ngorongoro si tu hifadhi, bali ni jukwaa la kidunia linalounganisha urithi, biashara na teknolojia sehemu moja.

Karibu Sabasaba timu yetu yenye wabobezi na watopezi imejipanga kukupa  hadhithi za Ngorongoro zitakazokuduwaza kuwa Ngorongoro sio mahali pa kuangalia tu, bali mahali pa kuelewa, kujifunza na kuishi uzoefu usiosahaulika.


Na Janeth Raphael MichuziTv 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, amesema maridhiano ya kisiasa hayapaswi kutafsiriwa kama udhaifu, bali ni ishara ya ukomavu wa kisiasa unaoweka msingi imara wa umoja, amani na kuheshimiana katika jamii.

Akihutubia katika hafla ya utiaji saini wa Tamko la Pamoja la Maridhiano ya Kisiasa Zanzibar iliyofanyika visiwani Zanzibar leo, Alhamisi Julai 9, 2026, Rais Samia alisema viongozi wanaweza kuwa na mitazamo tofauti, lakini wakaunganishwa na dhamira ya kulinda maslahi ya taifa na ustawi wa wananchi.

Ameeleza kuwa maridhiano yanaonyesha uwezo wa viongozi kujadili hoja zinazowatofautisha kwa hekima, huku wakikubaliana katika masuala ya msingi yanayohusu uongozi na maendeleo ya nchi.

Rais Samia alisema hatua hiyo inafungua ukurasa mpya wa kuimarisha umoja, mshikamano, utulivu na amani kwa wananchi wa Zanzibar na Tanzania kwa ujumla, akisisitiza kuwa jitihada hizo zinapaswa kuendelezwa na kuenziwa.

“Hakika jitihada hizi zinahitaji kuendelezwa na kuenziwa. Nimesema jambo hili la kiungwana kwa kuwa uungwana unatufunza siasa za kushindana kwa hekima na si kwa kupaza sauti bila mantiki,” amesema Rais Samia.

Aidha, ametoa wito kwa viongozi na wadau wa siasa kuendelea kujenga utamaduni wa mazungumzo, kuheshimiana na kuweka mbele maslahi ya taifa ili kudumisha amani na kuharakisha maendeleo ya wananchi.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na viongozi pamoja na wageni mbalimbali waliohudhuria hafla ya uwasilishaji wa Tamko la Pamoja la Muafaka wa Kisiasa baina ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na ACT-Wazalendo, katika viwanja vya Ikulu Zanzibar tarehe 09 Julai, 2026.







Na Mwandishi Wetu
USHIRIKIANO kati ya Serikali ya Tanzania na Serikali ya Japani kupitia Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Japani (JICA) umefungua fursa mpya za maendeleo katika sekta ya kilimo baada ya kutolewa kwa mkopo wa masharti nafuu wenye thamani ya zaidi ya Shilingi trilioni 3.5 kupitia Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB).

Fedha hizo zinatolewa kupitia Wizara ya Fedha chini ya mradi wa Two Step Loan, unaolenga kuongeza upatikanaji wa mitaji kwa sekta ya kilimo kwa kuwawezesha wakulima binafsi, vikundi vya wakulima pamoja na wakulima wadogo na wa kati kupata mikopo yenye masharti nafuu kwa ajili ya kuongeza uwekezaji na uzalishaji.

Akizungumza katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), Afisa Biashara wa TADB anayesimamia miradi ya benki hiyo, Elias Misana, alisema mradi huo unalenga kuchochea ukuaji wa sekta ya kilimo kupitia ufadhili wa mazao matano ya kimkakati ambayo ni mahindi, mpunga, ngano, alizeti na mazao ya bustani.

Alieleza kuwa kupitia mpango huo, mkulima mmoja mmoja ataweza kupata mkopo wa hadi Shilingi milioni 200, huku vikundi vya wakulima na kampuni zinazojihusisha na shughuli za kilimo zikiweza kukopa hadi Shilingi bilioni tatu kwa masharti nafuu.

Misana alisema mpango huo pia umeweka kipaumbele kwa wanawake na vijana wanaojishughulisha na kilimo cha bustani, ambao watanufaika na viwango vya chini vya riba pamoja na muda mrefu na rafiki wa marejesho ya mikopo.

Kwa upande wake, Mratibu Mkuu wa JICA, Veronica Barua, alisema mradi wa Two Step Loan ni matokeo ya ushirikiano wa muda mrefu kati ya Serikali ya Tanzania na Serikali ya Japani unaolenga kuwawezesha wakulima wadogo na wa kati kupata mitaji ya uwekezaji, hususan wale waliokuwa wakikabiliwa na changamoto ya kupata mikopo kutoka taasisi za kifedha.

Alisema upatikanaji wa mitaji hiyo unatarajiwa kuongeza tija katika uzalishaji wa mazao, kuboresha kipato cha wakulima na kuimarisha mchango wa sekta ya kilimo katika ukuaji wa uchumi wa taifa.

Mradi wa Two Step Loan ulianza kutekelezwa rasmi mwezi Juni mwaka 2025 na unatarajiwa kuendelea hadi mwaka 2029. Kupitia matawi ya TADB na benki washirika nchini kote, maelfu ya wakulima wanatarajiwa kunufaika na mpango huo, hatua itakayochochea usalama wa chakula, kuongeza uzalishaji na kuimarisha maendeleo ya sekta ya kilimo nchini.

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam,Albert Chalamila akipata maelezo kutoka kwa Afisa Mtendaji Mkuu wa Yas, Pierre Canton Bacara kuhusu huduma mbalimbali zinazotolewa na kampuni hiyo kwenye Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (SABASABA) mara baada ya kutembelea banda hilo, Banda la Yas limekusanya suluhisho mbalimbali zinazolenga kuboresha maisha ya Watanzania, ikiwemo huduma ya uchunguzi wa macho bure, mpango wa kumiliki simu janja na rauta za 5G kwa mkopo, huduma za intaneti majumbani na kwa wajasiriamali kupitia Yas Fiber, suluhisho kwa wafanyabiashara na taasisi kupitia Yas Business, pamoja na huduma na suluhisho mbalimbali za kifedha kupitia Mixx.
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Albert Chalamila akizungumza katika  kwenye Banda la Yas katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (SABASABA) wakati alipotembelea Banda hilo.
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Albert Chalamila akizungumza Mtoto aliyefika na mzazi wake kupata huduma ya Macho katika Banda la Yas  kwenye Banda la Yas katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (SABASABA) wakati Mkuu wa Mkoa huyo  alipotembelea Banda hilo.
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Albert Chalamila akizungumza na mwananchi   kwenye Banda la Yas katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (SABASABA) wakati alipotembelea Banda hilo.


Na Mwandishi Wetu
KAMISHNA wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya, Aretas James Lyimo, ameipongeza Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA) kwa mchango wake mkubwa katika kulinda afya ya wananchi kupitia usimamizi madhubuti wa ubora, usalama na ufanisi wa dawa pamoja na bidhaa nyingine za afya.

Kamishna Lyimo alitoa pongezi hizo alipotembelea banda la TMDA katika Maonesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, ambako alipata fursa ya kujionea huduma mbalimbali zinazotolewa na mamlaka hiyo pamoja na elimu inayotolewa kwa wananchi kuhusu matumizi salama ya dawa na bidhaa za afya.

Katika ziara hiyo, Kamishna Lyimo alipokelewa na Meneja wa Kitengo cha Mawasiliano na Elimu kwa Umma wa TMDA, Gaudensia Simwanza, ambaye alimueleza kuhusu majukumu ya mamlaka hiyo ya kusimamia ubora, usalama na ufanisi wa dawa, vifaa tiba, vitendanishi pamoja na bidhaa nyingine za afya kabla ya kufikishwa kwa watumiaji.

Akizungumza baada ya kutembelea banda hilo, Kamishna Lyimo alisema TMDA imeendelea kutekeleza wajibu wake kwa weledi, hatua inayochangia kuhakikisha Watanzania wanapata bidhaa za afya zilizo salama na zenye viwango vinavyokubalika.

Alisema usimamizi huo ni nguzo muhimu katika kulinda afya ya jamii na kuimarisha mapambano dhidi ya matumizi holela ya dawa pamoja na bidhaa nyingine zinazoweza kuhatarisha afya ya wananchi.

"TMDA ina jukumu kubwa katika kuhakikisha bidhaa za afya zinazowafikia wananchi zinakidhi viwango vya ubora, usalama na ufanisi. Hili ni jambo muhimu katika kulinda afya ya Watanzania na kuzuia matumizi yasiyo sahihi ya dawa," alisema.

Aidha, alisisitiza umuhimu wa kuendelea kuimarisha ushirikiano kati ya TMDA na Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya ili kuongeza ufanisi katika kudhibiti matumizi mabaya ya dawa na bidhaa nyingine zinazoweza kutumika kinyume cha sheria.

Kamishna Lyimo pia aliipongeza TMDA kwa kutumia Maonesho ya Sabasaba kama jukwaa la kuwafikia wananchi wengi kwa kutoa elimu kuhusu matumizi sahihi ya dawa, umuhimu wa kutumia bidhaa za afya zilizosajiliwa pamoja na tahadhari dhidi ya bidhaa zisizokidhi viwango.

Alieleza kuwa elimu hiyo ni nyenzo muhimu katika kujenga jamii yenye uelewa wa masuala ya afya, kupunguza madhara yatokanayo na matumizi yasiyo sahihi ya dawa na kuongeza ushiriki wa wananchi katika kulinda afya zao.

Kwa upande wake, TMDA imeendelea kutumia maonesho hayo kutoa huduma na elimu kwa umma kuhusu usalama wa dawa, vifaa tiba na bidhaa nyingine za afya, ikiwa ni sehemu ya juhudi zake za kuhakikisha wananchi wanapata bidhaa zilizosajiliwa na zinazokidhi viwango vya ubora kwa ajili ya kulinda afya na ustawi wa jamii.







Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) imetunukiwa tuzo ya kutambua mchango wake katika kufanikisha utafiti kuhusu maboresho ya kisasa ya mnyororo wa thamani wa kilimo uliofanywa na Taasisi ya Kimataifa ya Utafiti wa Maendeleo ya Canada (IDRC-CRDI) kwa kushirikiana na Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM).

Tuzo hiyo imekabidhiwa leo kwa Mkurugenzi Mtendaji wa WRRB, Bw. Asangye Bangu, na Meneja wa Kitengo cha Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) wa Bodi hiyo, Bw. Elfaraja Kintingu.

Akizungumza baada ya kupokea tuzo hiyo, Bw. Bangu amesema heshima hiyo ni uthibitisho wa nafasi muhimu ya WRRB katika kuimarisha sekta ya kilimo kupitia Mfumo wa Stakabadhi za Ghala, ambao umeendelea kuongeza ufanisi wa biashara ya mazao, uwazi wa masoko na ushindani wa bei katika masoko ya ndani na nje ya nchi.

Amesema WRRB itaendelea kushirikiana na taasisi za utafiti na wadau mbalimbali katika kuendeleza ubunifu na maboresho yanayochochea maendeleo ya mnyororo wa thamani wa kilimo kwa manufaa ya wakulima na uchumi wa Taifa.

Awali, akielezea kuhusu tuzo hiyo, Bw. Kintingu amesema imetolewa kwa kutambua ushirikiano na mchango wa WRRB katika kufanikisha utafiti huo, ambapo watafiti walitembelea ghala mbalimbali nchini ili kujionea utekelezaji wa Mfumo wa Stakabadhi za Ghala na mchango wake katika kuimarisha biashara ya mazao, kuongeza uwazi wa masoko na kuboresha mnyororo wa thamani wa kilimo.

Wanawake na mabinti nchini wamehimizwa kujitokeza kwa wingi kujiunga na kozi za ubaharia na fani nyingine zinazohusiana na uchumi wa bluu ili kunufaika na fursa nyingi za ajira na maendeleo zinazopatikana katika sekta hiyo.

Rai hiyo imetolewa na Mkufunzi Msaidizi wa Chuo cha Bahari Dar es Salaam (DMI), Winifrida Winsislaus Ngalu, wakati akizungumza na waandishi wa habari katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), Julai 8, 2026.

Amesema bado kuna dhana potofu miongoni mwa jamii kwamba fani za ubaharia ni za wanaume pekee, jambo ambalo si sahihi kwani wanawake wengi tayari wameingia katika sekta hiyo na wanaendelea kufanya vizuri katika nafasi mbalimbali.

Ngalu amesema Chuo cha Bahari Dar es Salaam kinashiriki maonesho hayo kwa lengo la kutoa elimu kuhusu fursa zinazopatikana kupitia kozi mbalimbali zinazotolewa chuoni hapo, pamoja na kuwahamasisha wananchi kujiunga na masomo yanayohusiana na uchumi wa bluu.

Aidha, amesema Serikali imeendelea kutoa kipaumbele kwa kozi zinazotolewa na chuo hicho, ambapo wanafunzi wanaojiunga kuanzia ngazi ya cheti wanaweza kupata mikopo hadi  elimu ya juu, hatua inayolenga kuongeza idadi ya wataalamu katika sekta hiyo muhimu.

Pia ameeleza kuwa chuo kinaendelea kupokea maombi ya wanafunzi wanaotaka kujiunga na programu za cheti na shahada za uzamili (Master’s Degree) pamoja na kozi za umahiri,  dirisha la maombi kwa awamu ya kwanza litafungwa Julai 10, 2026 na dirisha la ngazi ya Shahada yaani Digrii litafunguliwa Julai 15.

Ngalu ametoa wito kwa wanawake, mabinti na vijana kwa ujumla kutumia fursa hiyo kujiendeleza kielimu na kitaaluma, akisisitiza kuwa uchumi wa bluu una nafasi kubwa ya kuchangia ajira, ukuaji wa uchumi na maendeleo ya taifa.










Geneva, Julai 2026

Tanzania imelitaka Shirika la Miliki Ubunifu Duniani (WIPO) kujenga mfumo wa kimataifa wa miliki bunifu unaowezesha nchi zinazoendelea kunufaika na maendeleo ya akili mnemba (Artificial Intelligence–AI), huku ikisisitiza umuhimu wa kuhamasisha matumizi ya teknolojia na kujengea watu uwezo.

Akiwasilisha taarifa ya nchi kwa niaba ya Mhe Balozi Possi katika Mkutano wa 68 wa Nchi Wanachama wa Shirika la Miliki Ubunifu Duniani (WIPO) ulioanza tarehe 7 Julai, 2026 na kufanyika Geneva Uswisi, Naibu Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, Balozi Hoyce Temu, alisema miliki ubunifu imekuwa nyenzo muhimu ya kukuza ubunifu, viwanda na maendeleo ya uchumi.

"Tanzania inatambua miliki ubunifu kama kichocheo cha kimkakati cha ubunifu, uvumbuzi wa teknolojia, maendeleo ya viwanda na maendeleo endelevu ya kijamii na kiuchumi," alisema.

Alisema Tanzania inaendelea kujenga uchumi unaotegemea maarifa na inaiona akili mnemba kama fursa ya kuongeza kasi ya ubunifu na ukuaji wa uchumi.

"Tunaamini kuwa mifumo jumuishi ya miliki bunifu, ujenzi wa uwezo na uhamishaji wa teknolojia ni muhimu ili kuwezesha nchi zinazoendelea kunufaika kikamilifu na akili mnemba pamoja na teknolojia nyingine zinazoibuka," alisema.

Kauli hiyo inakuja wakati mataifa duniani yanaendelea kujadili namna mfumo wa miliki ubunifu utakavyoweza kuendana na kasi ya maendeleo ya akili mnemba. Nchi nyingi zinazoendelea zimekuwa zikitaka ushirikiano mkubwa zaidi katika uhamishaji wa teknolojia na maarifa ili kupunguza pengo la kidijitali.

Balozi Temu alisema Tanzania inaendelea kuimarisha mfumo wake wa miliki bunifu kupitia mageuzi ya sheria, kuboresha utoaji wa huduma, kuimarisha utekelezaji wa sheria, kujenga uwezo wa taasisi na kuongeza uelewa wa umma.

Aliishukuru WIPO kwa kuendelea kuiunga mkono Tanzania kupitia programu mbalimbali za kiufundi na ujenzi wa uwezo, ikiwemo kliniki za usimamizi wa haki miliki kwa biashara ndogo na za kati pamoja na kampuni changa, miradi ya uhamishaji wa teknolojia kupitia vyuo vikuu na taasisi za utafiti, mafunzo ya uchunguzi wa hataza na uwekaji wa mfumo wa kidijitali wa usimamizi wa haki miliki.

"Tunaendelea kujizatiti kuimarisha mfumo wa haki miliki ili uchangie zaidi katika ubunifu, uwekezaji, ujasiriamali, ajira na ukuaji endelevu wa uchumi," alisema.

Balozi Temu alisisitiza kuwa Tanzania itaendelea kushirikiana na WIPO pamoja na nchi nyingine wanachama kujenga mfumo wa haki miliki unaojumuisha wote, unaozingatia usawa na unaoweza kukidhi mahitaji ya teknolojia za sasa na zijazo.












Top News