

▪️︎ Azindua Mfumo wa Kitaifa wa Taarifa za Uwezeshaji Kiuchumi (NEMIS)
▪️︎ Ataka wigo wa miradi kwa Watanzania kupanuliwa
WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, ametoa wito wa kuhakikisha Watanzania wanashiriki kikamilifu katika uchumi wa nchi yao, akisisitiza kuwa uwezeshaji wa wananchi ni msingi wa kuongeza ajira, kukuza sekta binafsi, kuongeza mapato na kupunguza umaskini.
Dkt. Mwigulu ameyasema hayo leo (Alhamisi, Septemba 03, 2026) wakati akifungua Kongamano la Tano la Taifa la Ushiriki wa Watanzania katika Masuala ya Uchumi, lililofanyika Dodoma, lenye kaulimbiu inayosisitiza ushiriki wa Watanzania kama nguzo ya uchumi shindani na jumuishi kuelekea Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Amesema Serikali chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuweka mazingira ya kisera, kisheria na kiutendaji yatakayowawezesha Watanzania kushiriki moja kwa moja katika shughuli za kiuchumi, akisisitiza kuwa lengo si kuwazuia wawekezaji wa nje bali kuongeza uwezo na ushiriki wa Watanzania.
“Tuwawezeshe Watanzania kushika uchumi wao. Hii ndiyo njia ya kuongeza ajira, kuongeza vyanzo vya mapato na kujenga sekta binafsi yenye nguvu,” amesema.
Dkt. Mwigulu amesema Tanzania ina rasilimali nyingi na fursa kubwa za kiuchumi, hivyo ni muhimu kuhakikisha fursa hizo zinatafsiriwa kuwa ajira, biashara, uwekezaji na umiliki kwa Watanzania.Dkt. Mwigulu ameiagiza Wizara ya Fedha kuhakikisha marekebisho yanayofuata ya sheria za ununuzi yanaongeza wigo wa miradi inayoweza kutekelezwa na kampuni za Kitanzania.
Amesema kiwango cha Shilingi bilioni 50 kwa baadhi ya miradi kimekuwa kidogo kutokana na kukua kwa uchumi na uwezo wa kampuni za ndani, hivyo akapendekeza kiwango hicho kipandishwe hadi zaidi ya Shilingi bilioni 100 au Shilingi bilioni 150.
“Hii ya bilioni 50 imeshakuwa ya kawaida. Wekeni bilioni 100... au kama mnarekebisha sasa ikachukua muda, wekeni bilioni 150. Mambo yanaenda mbele. Tuwawezeshe Watanzania kushika uchumi wao,” amesema.
Amesisitiza pia kuwa fursa zinazotolewa na Serikali zinapaswa kutumiwa kwa uwajibikaji, akizitaka kampuni za Kitanzania kuhakikisha fedha za miradi zinatumika kutekeleza kazi kwa kiwango na ubora unaostahili, na kuonya kuwa Serikali haitasita kuchukua hatua dhidi ya watakaotumia vibaya fedha za umma.
Katika hatua nyingine, Dkt. Mwigulu amezindua rasmi Mfumo wa Kitaifa wa Taarifa za Uwezeshaji Kiuchumi (NEMIS) unaolenga kurahisisha upatikanaji wa taarifa kuhusu fursa mbalimbali za uwezeshaji kwa Watanzania.
Mfumo huo utasaidia kuwafikishia wananchi taarifa kuhusu fursa za mitaji kupitia mifuko na programu za uwezeshaji, zabuni za umma, fursa za uwekezaji pamoja na taarifa nyingine muhimu za kiuchumi.Dkt. Mwigulu amehitimisha kwa kusisitiza umuhimu wa kuondoka kwenye mipango na sheria na kuelekea kwenye utekelezaji unaoleta matokeo kwa wananchi.
“Tanzania inasifika sana kwa mipango mizuri, inasifika sana kwa sheria hizi hizi tunazoziandika. Sasa tupige hatua twende kwenye kuhakikisha haya tunayotekeleza, haya tunayopanga, haya tunayoyaandika yanaonekana kwenye vitendo.”
Akizungumza katika kongamano hilo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Prof. Palamagamba Kabudi, amesema Serikali imeendelea kuweka mifumo, sera na sheria zinazolenga kuongeza ushiriki wa Watanzania katika uchumi, akisisitiza umuhimu wa uratibu ili fursa hizo ziwafikie wananchi na kuongeza ushiriki wao katika shughuli za kiuchumi.
Kwa upande wake, Waziri wa Madini, Anthony Mavunde, amesema manunuzi ya bidhaa na huduma katika sekta ya madini yanafikia Shilingi trilioni 5.1 kwa mwaka, ambapo Serikali imehakikisha asilimia 90 ya manunuzi hayo yanabaki nchini Tanzania, hatua inayoongeza ushiriki wa Watanzania katika mnyororo wa thamani wa sekta hiyo.
Kwa niaba ya Bunge, Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Edwin Swale, amesema Bunge limeendelea kuunga mkono hatua za Serikali za kuwawezesha wananchi kiuchumi kupitia maboresho ya sheria, akibainisha kuwa Serikali imeweka mifuko zaidi ya 74 ya uwezeshaji na imeendelea kuchukua hatua za kupunguza vikwazo kwa wafanyabiashara na wajasiriamali.
Nae, Mwenyekiti wa Baraza la Taifa la Uwezeshaji Kiuchumi, Prof. Aurelia Kamuzora, amesema uwezeshaji wa wananchi unapaswa kwenda sambamba na kujenga uwezo wa watu, upatikanaji wa mitaji, taarifa na ujuzi ili Watanzania waweze kushindana ndani na nje ya nchi.
Amesema Baraza limeweka mkazo katika kuwafikishia wananchi taarifa za fursa za kiuchumi na kuimarisha vituo vya uwezeshaji katika mikoa na wilaya.
-Yazindua bidhaa tatu za Jubilee Life Insurance ambazo ni Fanaka Plus, Smart Education Insurance Plan na Akiba Flex Plan
Na Said Mwishehe, Michuzi TV
MAMLAKA ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) imezitaka kampuni za bima kubuni bidhaa zinazotoa majibu ya vitendo kwa changamoto zinazowakabili wananchi, ikisema ubora wa bidhaa za bima haupaswi kupimwa kwa idadi ya watu waliojiunga pekee.
Kamishna wa Bima, Dk.Baghayo Saqware amesema kampuni zinazolenga kuongeza ujumuishi wa kifedha zinapaswa kwanza kuelewa mazingira wanamoishi Watanzania na changamoto zinazowakabili kabla ya kubuni bidhaa zinazokidhi mahitaji yao.
Dk.Saqware ametoa kauli hiyo katika hotuba iliyosomwa kwa niaba yake na Mkurugenzi wa Uzingatiaji wa Sheria na Kanuni wa TIRA, Bw Alex Rock wakati wa uzinduzi wa bidhaa tatu mpya za bima ya maisha za Jubilee Life Insurance Tanzania uliofanyika leo Septemba 3,2026 jijini Dar es Salaam.
“Mwito wangu kwa Jubilee Life Insurance na kampuni nyingine za bima ni kuendelea kubuni bidhaa zinazotoa majibu kwa changamoto za wananchi na kuboresha maisha yao,” amesema Dk Saqware.
“Ubora wa bidhaa haupimwi kwa idadi ya watu waliojiunga pekee. Uelewa hujenga imani, na imani huongeza matumizi endelevu ya bima,”amesema na kuongeza Tanzania inaingia katika hatua muhimu ya kujenga familia zenye uwezo wa kustahimili misukosuko ya kifedha na taifa lenye uimara wa kifedha huku bima ya maisha ikiwa na nafasi muhimu katika kulinda wananchi na kusaidia mipango yao ya muda mrefu.
Ameongeza Jubilee Life Insurance kwa kuwasilisha bidhaa hizo kwa lugha ya Kiswahili, akisema matumizi ya lugha inayoeleweka kwa urahisi ni muhimu katika kuongeza uelewa na ujumuishi katika huduma za bima.
“Matumizi ya lugha inayoeleweka katika kutoa taarifa na elimu kuhusu bima huwawezesha wananchi kuelewa kwa usahihi faida, masharti na wajibu wao kabla na baada ya kujiunga na bima,” alisema.
Dk.Saqware amesema pia bima ya maisha ni nyenzo muhimu katika kujenga usalama wa kifedha na uwezo wa kustahimili changamoto kwa mtu binafsi, familia na taifa kwa ujumla.
Amesisitiza bima hiyo hulinda kipato na mipango ya maisha dhidi ya athari za kifo, ulemavu, maradhi, ajali na matukio mengine yasiyotarajiwa, huku pia ikiwasaidia wananchi kuweka akiba kwa ajili ya mahitaji muhimu ya baadaye, yakiwemo elimu ya watoto na ustawi wa familia.
“Bila ulinzi wa bima, tukio lisilotarajiwa linaweza kukatisha elimu ya watoto, kuathiri maisha ya familia na hata kuzima ndoto za wanufaika,” alisema.Kupitia bima ya maisha, ndoto na mipango hiyo inaweza kulindwa na kuendelea kuwa halisi.”
Pia amesema matumizi ya bima ya maisha nchini bado hayajafikia kiwango kinachotarajiwa, huku baadhi ya sababu zikitajwa kuwa ni aina na muundo wa bidhaa zinazopatikana sokoni pamoja na uwezo wake wa kujibu mahitaji halisi ya wananchi.
Pamoja na hayo amesema uzinduzi wa bidhaa hizo unaendana na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayolenga kujenga uchumi imara, jumuishi na wenye uwezo wa kustahimili misukosuko.
Amesema hatua hiyo pia inaunga mkono Mpango Mkuu wa Maendeleo ya Sekta ya Fedha wa mwaka 2020–2030, ambao unalenga kuongeza mchango wa bima ya maisha katika pato la taifa hadi kufikia asilimia 3 ifikapo mwaka 2030.
Kwa upande wake Ofisa Mtendaji Mkuu wa Jubilee Life Insurance Tanzania Helena Mzena amesema kampuni hiyo imeendelea kuboresha bidhaa zake ili kuwapatia wateja thamani na uhakika zaidi.
Amesema Fanaka Life Plan imeboreshwa na kubadilishwa jina kuwa Fanaka Plus, ikiwapa wateja fursa ya kukuza fedha zao huku wakipata ulinzi wa maisha na amani ya moyo.
Ameongeza kuwa Akiba Flex inawapa wateja uhuru zaidi wa kuweka michango na kufanya miamala ya fedha kulingana na mahitaji yao.
Aidha, amesema Smart Education Insurance Plan imeundwa mahsusi kuwasaidia wazazi na walezi kujiandaa kwa ajili ya elimu ya watoto wao.“Hapa, mteja anaweza kuweka akiba ili kuhakikisha ndoto za kielimu za watoto wake zinatimia, huku pia akiwa na ulinzi wa maisha.
“Bidhaa hizi za bima ni ushahidi kwamba tunajali na kuthamini ndoto za wateja wetu na tunataka kuhakikisha ndoto hizo zinatimia bila msongo usio wa lazima.”
Wakati huo huo Mwenyekiti wa Bodi ya Jubilee Insurance Amyn Lalji amesema uzinduzi huo ni hatua nyingine muhimu katika safari ya Jubilee Life Insurance Tanzania na unaakisi dhamira ya kampuni hiyo ya kutoa suluhisho bunifu na la vitendo linalokidhi mahitaji yanayobadilika ya Watanzania.
MAKAMU wa Rais wa Tanzania, Deogratius Ndejembi, ametoa maeekezo kwa Wizara ya Viwanda na Biashara kukaa meza moja na wazalishaji wa saruji nchini ili kuweka mikakati ya haraka itakayohakikisha saruji inapatikana kwa wingi na bei nafuu.
Ametoa maelekezo jijini Dar es Salaam alipokuwa katika hafla ya utoaji wa Tuzo za Rais kwa Mzalishaji Bora Viwandani (President’s Manufacturer of the Year Awards - PMAYA), zinazoratibiwa na Shirikisho la Wenye Viwanda Tanzania (CTI).
Akieleza kero ya wananchi kuhusu gharama za ujenzi, Makamu wa Rais amesema kwamba wananchi wanalazimika kununua saruji kwa bei kubwa kutokana na usimamizi na uratibu dhaifu wa uzalishaji viwandani, jambo ambalo linaenda kinyume na maelekezo ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Kutokana na bei ya saruji kuwa juu Makamu wa Rais Ndejembi amesema” Nakuagiza Waziri wa Viwanda na Biashara, Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda pamoja na Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), kaeni mmalize hili suala ili mwananchi apate saruji kwa bei iliyokuwepo awali.
Amesisitiza baada ya Wizara hiyo kukaa anataka kupata ripoti kuhusu jambo hilo huku akiwataka wajadili na kisha mwandike ripoti ambayo itakabidhiwa kwa Rais Dk.Samia Suluhu Hassan.
Na Mwandishi Wetu.
NMB Foundation (NMBF), ikishirikiana na Benki ya NMB, imetenga Sh bilioni 1 kuwawezesha vijana hao kupitia dirisha la tatu la programu ya Nuru Yangu Scholarship and Mentorship kwa mwaka wa masomo 2026/27.
Maombi yote yatapokelewa kupitia tovuti ya NMB Foundation, foundation.nmbbank.co.tz, kuanzia leo hadi tarehe 18 Septemba 2026.
Programu hiyo inalenga Watanzania waliomaliza Kidato cha Sita mwaka huu kwa Daraja la Kwanza lenye pointi tatu hadi tano. Waombaji pia wanapaswa kuwa na ushahidi wa uhitaji wa kifedha na kutarajia kujiunga na taasisi za elimu ya juu zinazotambuliwa nchini.
Akizungumza jijini Dar es Salaam, Meneja Mkuu wa NMB Foundation, Nelson Karumuna, alisema vijana watakaochaguliwa wataungana na wanufaika 101 waliowezeshwa kupitia awamu mbili zilizopita.
Kwa kuongezwa vijana hao 50, idadi ya wanufaika wa programu hiyo itafikia 151. NMBF imetumia zaidi ya Sh bilioni 2.1 katika awamu zilizopita, huku Sh bilioni 1 zikitengwa kwa kundi jipya.
“Uwezeshaji huu utagharamia ada, fedha za kujikimu, mafunzo kwa vitendo, malipo ya lazima ya chuo na vifaa vya kujifunzia, ikiwemo kompyuta mpakato,” alisema Karumuna.
Alisema vijana watakaopatikana pia watapatiwa malezi na ushauri wa kitaaluma, mafunzo ya uongozi, maandalizi ya kuingia katika soko la ajira na fursa za kujifunza kwa vitendo.
Karumuna alisisitiza kuwa maombi hayana gharama na hakuna mtu wala taasisi iliyopewa mamlaka ya kuuza nafasi hizo. Uchaguzi utafanywa kwa kuzingatia vigezo vilivyowekwa na uhakiki wa kina ili kuhakikisha fursa zinawafikia walengwa.
Programu ya Nuru Yangu ilianzishwa Mei 19, 2022, ikiwa na lengo la kuondoa vikwazo vya kifedha vinavyowazuia vijana wenye uwezo mkubwa kitaaluma kuendelea na elimu ya juu.
Mmoja wa wanufaika wake, Elia Johnson Kaberege, aliyehitimu Shahada ya Uhasibu katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam mwaka 2025, alisema programu hiyo ilimwezesha kumudu gharama za masomo na mahitaji mengine ambayo familia yake isingeweza kugharamia.
Naye Irene John Busorwa, mhitimu wa Chuo Kikuu Mzumbe, alisema alikaribia kukosa nafasi ya kujiunga na chuo kutokana na hali ya kifedha ya familia yake. Kupitia Nuru Yangu, aliweza kusoma kwa miaka mitatu na kuhitimu. Kwa sasa ameajiriwa katika kampuni ya ukaguzi wa hesabu.
NMBF, ikishirikiana na Benki ya NMB, imewataka vijana wenye sifa kutuma maombi kupitia tovuti rasmi pekee kabla ya kufungwa kwa dirisha hilo Septemba 18, 2026.

Akizungumza katika hafla hiyo, Makamu wa Rais ametoa wito kwa Wizara ya Viwanda na Biashara kwa kushirikiana na wazalishaji wa saruji nchini, kuhakikisha wanatafuta suluhu ya haraka ili kurejesha bei ya kawaida ya saruji kwa wananchi. Amesema maono ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ni kuona wananchi wanaweza kununua mfuko wa saruji kwa gharama nafuu hivyo ni lazima kuoanisha uzalishaji wa malighafi zote zinazochangia katika uzalishaji wa saruji ili bidhaa hiyo ipatikane kwa urahisi.
Halikadhalika, Makamu wa Rais amesema ni muhimu kufanya tathimini ya ukuaji wa viwanda hapa nchini ili kutambua ukuaji huo kama unaviwezesha viwanda kuwa na ushindani wa masoko katika kanda, Afrika na Dunia kwa ujumla.
Makamu wa Rais amesema Serikali itaendelea kuchukua hatua kali za kisheria kwa wafanyabishaara wote wanaojihusisha na biashara haramu za uingizaji bidhaa bandia ambazo hukwepa kodi na tozo mbalimbali stahiki ambapo, zinaathiri ukuaji wa viwanda, kusababisha upotevu wa mapato ya serikali pamoja na kupunguza ushindani wa bidhaa zinazozalishwa ndani ya nchi.
Amewataka wazalishaji wa viwandani hapa nchini, kufanya jitihada za kuongeza uchakataji wa malighafi ndani ya nchi kwa kuhakikisha wanaongeza thamani, hatua itakayosaidia katika kuongeza ajira kwa watanzania na ukuaji wa uchumi kwa kasi.
Aidha, Makamu wa Rais ameitaka Wizara ya Viwanda na Biashara kuhakiki takwimu sahihi za idadi ya viwanda vilivyopo ili kuweka mikakati ya namna ya kuongeza wanachama wa Shirikisho la Viwanda Tanzania, hali itakayorahisisha uwepo wa chombo kimoja kinachowawakilisha wazalishaji wa viwandani.
Makamu wa Rais amesema katika kukuza uchumi na kuboresha maisha ya watanzania, sekta ya viwanda ina nafasi kubwa kwa kuwa ndiyo chimbuko la maendeleo ya haraka na ni muhimili mkuu katika uongezaji thamani wa malighafi zilizopo, utoaji ajira kwa wananchi, kuongeza mapato ya Serikali pamoja na fedha za kigeni. Pia, amesema sekta ya viwanda ni muhimu katika kuboresha sayansi na teknolojia na kuongeza uzalishaji, na hivyo kukuza ubunifu, uvumbuzi, uchumi, na kuondoa umasikini nchini.
Amesema kutokana na wingi wa rasilimali zilizopo nchini ikiwemo misitu na madini mbalimbali, ni muhimu kukuza sekta ya viwanda na kuendelea kujenga mahusiano kati ya sekta ya viwanda na nyingine ili kuongeza ufanisi, kuharakisha maendeleo jumuishi na hatimaye kuongeza kipato cha Watanzania walio wengi.
Makamu wa Rais amesema Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan itaendelea kufanya kazi kwa karibu na sekta binafsi ili kuharakisha maendeleo ya Taifa.
Kwa upande wake Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Judith Kapinga, amesema Wizara hiyo imeendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ili kuhakikisha lengo lake la kuendeleza sekta ya viwanda linafanikiwa. Amesema Sekta hiyo imeendelea kujiimarisha ili kuongeza nafasi katika mchango wa pato la Taifa na kuongeza ufanisi kwa lengo la ukuaji wa sekta hiyo muhimu.
Amesema tayari Wizara imekamilisha na itazindua Sera ya Maendeleo endelevu ya Viwanda ya Mwaka 2025 na Sera ya Maendeleo ya jasiriamali ndogo na za kati ya mwaka 2003 Toleo la mwaka 2025 ikiwa na lengo la kwenda sambamba na Dira 2050 ambayo inategemea uendelevu wa Viwanda.
Mwenyekiti wa Shirikisho la Viwanda Tanzania (CTI) Hussein Suphian Ally ameipongeza Serikali kwa mafanikio mbalimbali yanayoendelea kuimarisha mchango wa sekta ya viwanda nchini ikiwemo uwekezaji mkubwa unaofanywa katika miradi ya kimkakati ambayo imeendelea kuongeza ushindani katika sekta ya viwanda.
Amesema CTI inapongeza juhudi za Serikali za kuendelea na ujenzi wa miradi ya Reli ya Kisasa (SGR), ujenzi na upanuzi wa Bandari, ujenzi wa mitandao ya barabara pamoja na uwekezaji katika nishati na miundombinu mingine ya kiuchumi ambayo kwa pamoja imeendelea kupunguza gharama za usafirishaji, kurahisisha biashara na kuongeza uwezo wa bidhaa zinazozalishwa nchini kufikia masoko ya ndani, kikanda na kimataifa.
Katika hafla hiyo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amezawadia tuzo ya heshima kwa kutambua mchango wake katika uboreshaji wa mazingira ya uwekezaji na viwanda nchini.
Hafla hiyo imewakutanisha wazalishaji wakubwa, wakati na wadogo, wafanyabiashara pamoja na wadau wengine wa sekta ya viwanda na biashara, huku tuzo hizo zikiendelea kuwa jukwaa la kuhamasisha ubora, ubunifu, uwekezaji, matumizi ya teknolojia na uzalishaji endelevu nchini.



.jpeg)


.jpeg)








.jpeg)

.jpeg)




.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)



.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)








