KAMPENI maalumu ya Darling Hair maarufu kama Loyalty Program, imezidi kushika kasi huku wasusi mbalimbali nchini wakiendelea kunufaika kwa njia mbalimbali wakati program hiyo ikiadhimisha miaka miwili tangu kuanzishwa kwake.

Wasusi mbalimbali wakizungumza katika sherehe maalulu iliyofanyika Gongo la Mboto na kuwakusanya wasusi mbalimbali katika kuadhimisha miaka miliwi ya program hiyo, waliipongeza Darling Hair kwa kuwajali na kuwawezesha kiuchumi kwa kuwapa vifaa baada ya kujizolea pointi kutokana na kukusanya lebo za bidhaa za kampuni hiyo.

“Siku ya leo imekuwa muhimu sana kwetu kama wasusi kwa sababu tumekutana na kubadilishana mawazo, tumepata mafunzo na pia vifaa mbalimbali vya saluni kutoka Darling Hair. Kwa kweli hawa hawana mpinzani,” alisema Jackline Temba ambaye anamiliki saluni eneo la Kitunda Jijini Dar es Salaam.

Alitoa wito kwa wasusi ambao hawajajiunga na program hiyo ya loyalty kufanya hivyo ili nao wafaidike na wajinyanyue kiuchumi.

Naye Regina Filbert kutoka Kitunda alisema kupitia program hiyo wasusi wamejifunza mambo mengi kutokana na mafunzo ya mara kwa mara na pia wamejishindia zawadi nyingi katika miaka miwili ya kampeni hii.

“Binafsi kupitia kampeni hii nimeshinda viti, rollers na vifaa vingine baada ya kukusanya lebo hizi na kukusanya pointi zilizoniwezesha kushinda,” alisema.

Salumu Hamisi, maarufu kama DD kutoka eneo la Banana, alisema Darling Hair imekuwa familia kwa wasusi na imekuwa ikiwafuatilia kwa karibu mno ili kuhakikisha wanashugulikia changamoto zozote na wasusi wote wanafikiwa wakubwa kwa wadogo.

“Wamekuwa ni wasikivu sana na wanatufuatilia kwa karibu. Changamoto zetu nyingi tu wameshazishugulikia ndio maana bidhaa zao zinaendelea kuongoza sokoni,” aliongeza.

Alitoa wito kwa wasusi mbalimbali kuangalia vifaa wanavyohitaji na kujiunga na program hiyo ili washinde na kujiongezea mitaji ili wafanye boashara kwa wepesi.

Mwakilishi wa Darling Hair, Daniel Kisusange kutoka idara ya Masoko, alisema hafla hii iliwakutanisha wasusi kutoka Gongo la Mboto, Chanika, Pugu, Banana, Kitunda na maeneo mengine.

“Tulianzisha program hii ili turudishe kwa wateja wetu wakubwa ambao ni wasusi lakini pia tuliona umuhimu wa kuwakusanya wasusi wote pamoja ili wabadilishane mawazo na kupata ujuzi na maarifa mapya,” alisema.

Aliongeza kuwa hadi sasa wameshawafikia wasusi zaidi ya 10,000 na kufikia mwakani wanatarajia wasusi hawa wataongezeka maradufu. “Baada ya Dar es Salaam tutaelekea mikoani na tutapia Tanga, arusha, Morogoro, Dodoma, Iringa, Shinyanga na Geita,” alisema.

Baraza la Mitihani la Tanzania (NECTA) limetangaza kuwa Mtihani wa Kumaliza Elimu ya Msingi (PSLE) kwa mwaka 2026 utafanyika Septemba 9 na 10, ukihusisha watahiniwa 1,168,649 kutoka shule 20,019 nchini.

Katibu Mtendaji wa NECTA, Prof. Said A. Mohamed, amesema kati ya watahiniwa hao, wavulana ni 531,467 sawa na asilimia 45, huku wasichana wakiwa 637,182 sawa na asilimia 55.

Amesema watahiniwa 1,081,204 sawa na asilimia 93 watafanya mtihani kwa Kiswahili, huku 87,445 sawa na asilimia saba wakifanya kwa lugha ya Kiingereza.

Kwa mujibu wa Prof. Mohamed, watahiniwa wenye mahitaji maalumu 4,867 pia wamesajiliwa kufanya mtihani huo. Kati yao, 82 ni wasioona, 1,591 wenye uoni hafifu, 999 wenye uziwi, 576 wenye ulemavu wa akili na 1,619 wenye ulemavu wa viungo.

Amesema masomo yatakayotahiniwa ni Kiswahili, English Language, Sayansi na Teknolojia, Hisabati, Maarifa ya Jamii na Stadi za Kazi, pamoja na Uraia na Maadili.

Prof. Mohamed amesema mtihani huo ni wa mwisho kufanyika kwa kutumia mtaala wa sasa, huku ukilenga kupima maarifa na ujuzi walioupata wanafunzi katika miaka saba ya elimu ya msingi na kutumika katika mchakato wa uchaguzi wa wanafunzi wanaojiunga na elimu ya sekondari.

Amesema maandalizi yote ya mtihani huo yamekamilika, yakiwemo usambazaji wa karatasi za mitihani na nyaraka muhimu katika halmashauri zote nchini, mafunzo kwa wasimamizi pamoja na kuweka mikakati ya kuhakikisha usalama wa vituo vya mitihani.

Amewataka wasimamizi wa mitihani kutekeleza majukumu yao kwa uadilifu na kuzingatia kanuni za mitihani, huku wakihakikisha watahiniwa wote wanapata fursa ya kufanya mtihani kwa muda uliopangwa.

Kwa watahiniwa wenye mahitaji maalumu, amesema NECTA imeweka utaratibu wa kuwapatia maandishi ya nukta nundu kwa wasioona, maandishi yaliyokuzwa kwa wenye uoni hafifu na muda wa ziada wa dakika 20 kwa kila saa katika somo la Hisabati na dakika 10 kwa kila saa kwa masomo mengine.

Aidha, amewataka watahiniwa kuepuka vitendo vya udanganyifu, akisisitiza kuwa matokeo ya mwanafunzi atakayebainika kufanya udanganyifu yatafutwa kwa mujibu wa kanuni.

Amewataka wamiliki na wakuu wa shule kutokuingilia majukumu ya wasimamizi wakati wa mtihani, akionya kuwa NECTA inaweza kufuta kituo cha mtihani endapo itabaini uwepo wake unahatarisha usalama wa mtihani.

Pia ameitaka jamii kutoa ushirikiano kwa kuhakikisha mitihani inafanyika kwa amani na utulivu, ikiwemo kuheshimu maeneo ya mitihani na kuepuka kuingia shuleni wakati wa uendeshaji wa mtihani.

NECTA imetoa wito kwa wananchi kutoa taarifa za vitendo vya udanganyifu kupitia namba 0759 360 000 au barua pepe esnecta@necta.go.tz.

Mtihani huo utafanyika Jumatano, Septemba 9, na Alhamisi, Septemba 10, 2026.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, ameipongeza Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) kwa kusimamia Uchaguzi Mkuu wa Zanzibar wa mwaka 2025 kwa amani na utulivu.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, tarehe 08 Septemba 2026, Ikulu Zanzibar, wakati akikabidhiwa Ripoti ya Uchaguzi Mkuu wa Zanzibar wa mwaka 2025 na Mwenyekiti wa ZEC, Mhe. Jaji George Joseph Kazi.

Amesema Serikali na ZEC zinapaswa kuendelea kushirikiana kutatua changamoto zilizojitokeza katika uchaguzi huo ili zisijirudie katika chaguzi zijazo.

Aidha, ameipongeza ZEC kwa kuongezeka kwa idadi ya wapiga kura walioandikishwa kutoka 566,352 mwaka 2020 hadi 717,557 mwaka 2025, sawa na ongezeko la asilimia 26.7, pamoja na Serikali kugharamia uchaguzi huo kwa asilimia 100 kwa mara ya kwanza.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa ZEC, Mhe. Jaji George Joseph Kazi, amesema mafanikio mengine ni kuendelea kutumia Tactile Ballot Folder kuwawezesha watu wenye ulemavu wa kuona kupiga kura bila msaada, pamoja na kupatikana kwa jengo la kisasa la One Stop Center na majengo sita ya Afisi za Uchaguzi za Wilaya.

Vilevile, Rais Dkt. Mwinyi ameishukuru ZEC kwa kazi iliyofanyika na kuwataka viongozi na watendaji wake kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa uadilifu na weledi, huku Serikali ikiendelea kushirikiana na Tume kuimarisha mazingira ya chaguzi zijazo.












Mbogwe, Geita


‎Serikali kupitia Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) imetenga kiasi cha shilingi bilioni 3.6 kwa ajili ya kulipa fidia wananchi 554 wanaoathiriwa na ujenzi wa barabara zenye urefu wa kilomita 58 kwa kiwango cha lami wilaya ya Mbogwe mkoani Geita.

‎Zoezi hilo linahusisha wananchi ambao mali zao ikiwemo nyumba, mazao na maeneo mengine zimeathiriwa na utekelezaji wa mradi huo unaolenga kuboresha miundombinu ya usafirishaji na kuchochea shughuli za kiuchumi na kijamii katika wilaya ya Mbogwe.

‎Akizungumza wakati akitoa taarifa kuhusu utekelezaji wa zoezi hilo, Meneja wa TARURA wilaya ya Mbogwe Mhandisi Patrick Chacha amesema tathmini ya mali za wananchi wanaoathiriwa na mradi imefanyika kwa lengo la kuhakikisha wanapata stahiki zao kabla ya kupisha utekelezaji wa mradi.

‎Mhandisi Chacha amesema ulipaji wa fidia ni sehemu muhimu ya utekelezaji wa mradi kwani unalenga kuwawezesha wananchi wanaoathiriwa na mradi kurejesha maisha yao na kuendelea na shughuli zao baada ya kupisha ujenzi wa barabara.

‎"Serikali chini ya uongozi wa Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imetenga kiasi hiki cha fedha ili kuwezesha wananchi kujenga nyumba mpya na kuendelea na maisha yao baada ya kuondolewa makazi yao ya awali kwa ajili ya kupisha ujenzi wa barabara", amesema Mhandisi Chacha.

‎Aidha, Mhandisi Chacha amesema wilaya ya Mbogwe ni miongoni mwa maeneo yatakayopata manufaa makubwa kutokana na mradi huo akieleza kuwa ujenzi wa kilomita 58 kwa kiwango cha lami utaboresha usafiri na usafirishaji, huku ukifungua fursa mpya za biashara na kuongeza thamani ya shughuli za kiuchumi kwa wananchi.

‎Amesema barabara hizo zitakapokamilika zitasaidia kurahisisha usafirishaji wa bidhaa na mazao, kupunguza changamoto za usafiri na kuongeza ufanisi wa shughuli mbalimbali za kijamii na kiuchumi.

‎Kwa upande wake, Mwenyekiti wa kijiji cha Kabanga Bw. Joseph Masanja amesema zoezi la tathmini ya mali za wananchi katika eneo lake limefanyika kwa ufasaha huku wananchi wakieleza kuridhishwa na hatua zinazochukuliwa na serikali katika kuhakikisha wanapata fidia zao.

‎Masanja amesema awali baadhi ya wananchi walikuwa na mashaka kuhusu uwezekano wa utekelezaji wa mradi huo lakini hatua iliyofikiwa sasa imewapa matumaini makubwa.

‎"Mwanzoni watu walidhani suala hili haliwezekani lakini sasa tumefikia hatua ya mwisho ya kulipwa fidia na kila mmoja wetu anapongeza jitihada za serikali", amesema.

‎Ametoa wito kwa wananchi wa Kabanga na maeneo mengine ya Mbogwe kutumia fursa zitakazojitokeza baada ya kukamilika kwa mradi huo hususan katika biashara, kilimo, usafirishaji na huduma mbalimbali.

‎Mradi wa ujenzi wa barabara hizo unatekelezwa na TARURA kupitia mradi wa RISE unaogharamiwa na mkopo nafuu toka Benki ya Dunia.







Bodi ya Wakurugenzi ya INADES Formation Tanzania imefanya kikao chake cha kwanza tangu ichaguliwe mwezi Mei, kikilenga kupitia utekelezaji wa bajeti na shughuli za taasisi kwa kipindi cha Januari hadi Juni 2026, pamoja na kujadili mipango ya utekelezaji kwa kipindi cha Julai hadi Desemba 2026.

Akizungumza Mwenyekiti wa Bodi hiyo, Alphonce Katunzi, Jijini Dodoma, amesema lengo ni kuhakikisha kuwa mipango ya taasisi inaendana na mahitaji halisi na kwamba rasilimali zilizopo zinatumika kwa ufanisi katika kutekeleza majukumu na kufikia matokeo yaliyokusudiwa.

Amesema taasisi hiyo inataka kuendelea kuboresha namna inavyotekeleza shughuli zake, ikiwemo kuhakikisha huduma na programu zinazotolewa zinaendana na mahitaji ya jamii na wanufaika, kwa kuzingatia mfumo unaoangalia mahitaji halisi.

Amesema kikao hicho pia kimejadili na kupitisha makadirio ya bajeti ya mwaka 2027, huku kikifanya tathmini ya utekelezaji wa bajeti ya mwaka 2026 kwa kipindi cha Januari hadi Juni na kuangalia mipango ya utekelezaji kwa kipindi kilichobaki cha mwaka.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa INADES Formation Tanzania, Jacquline Nicodemas, amesema kabla ya kikao cha bodi, kwa takribani siku tatu kulifanyika vikao vya kiutendaji na kimaamuzi, ikiwemo vya Kamati ya Fedha, Rasilimali Watu na Utendaji Kazi pamoja na Kamati ya Mafunzo na Afya ya Jumuiya.

Amesema vikao hivyo ni sehemu ya kuimarisha utawala bora, uwajibikaji na utendaji wa taasisi, huku akieleza kuwa katika kipindi cha hivi karibuni taasisi imetekeleza programu kuu mbili zilizosaidia kuimarisha ushirikiano na Serikali, wadau mbalimbali pamoja na jamii, ikiwemo kuongeza fursa za kiuchumi kwa wananchi.

Naye Makamu Mwenyekiti wa Bodi, Specioza Kifuto, amesema baada ya kikao hicho wanatarajia wanajumuiya na wadau kuanza kuona mabadiliko katika utekelezaji wa shughuli za taasisi, ikiwemo kuboreshwa kwa huduma zinazotolewa kwa wakulima na jamii kwa ujumla, amesisitiza wadau kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wa shughuli, kutumia mafunzo wanayopata katika vitendo na kushiriki katika kutekeleza maamuzi yaliyokubaliwa.








Na Vero Ignatus Michuzi Tv Arusha

Tanzania imepiga hatua nyingine katika kujiweka tayari kwa ulinzi na usalama kuelekea Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2027, baada ya kufungwa kwa mafunzo maalum ya siku tano mkoani Arusha yaliyolenga kuimarisha usalama wa nyuklia na mionzi.

​Mafunzo hayo yaliyoandaliwa na Tume ya Nguvu za Atomiki Tanzania (TAEC) kwa kushirikiana na Wakala wa Kimataifa wa Nguvu za Atomu (IAEA), yalihusisha vyombo vya ulinzi na usalama pamoja na taasisi mbalimbali nchini ili kujenga uwezo wa kuzuia, kutambua na kukabiliana na vitisho wakati wa mashindano hayo.

​Akifunga mafunzo hayo ya siku tano Jijini Arusha Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam na Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya AFCON 2027, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Muliro J. Muliro, alisema kuwa maandalizi hayo ni chachu ya kuhakikisha nchi inakuwa na mifumo madhubuti ya kiusalama.

​SACP Muliro aliwataka washiriki kutumia maarifa waliyopata kufanya tathmini katika taasisi zao ili kubaini uwezo uliopo na kufanyia kazi mapungufu mapema, akisisitiza kuwa ukubwa wa mashindano ya AFCON 2027—yatakayoandaliwa kwa pamoja kati ya Tanzania, Kenya na Uganda—unahitaji maandalizi ya kina.

​Mafunzo hayo yalichanganya nadharia za darasani na mazoezi ya vitendo, ikiwa ni pamoja na zoezi la kutafuta na kutambua chanzo bandia cha mionzi kilichokuwa kimefichwa. Zoezi hilo lilipima uwezo wa washiriki katika kutumia vifaa, maarifa na taratibu za kiusalama walizofundishwa katika mazingira halisi.

​Kwa upande wa sekta ya michezo, Alex Mkenyenge kutoka Idara ya Michezo, Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, alieleza kuwa usalama wa viwanja na maeneo ya michezo ni nguzo kuu ya maandalizi hayo.

​"Serikali imefanya uwekezaji mkubwa katika ujenzi na uboreshaji wa viwanja vya mechi na mazoezi jijini Dar es Salaam, Arusha na Zanzibar. Ni muhimu kuhakikisha miundombinu hii na watu watakaoitumia wanalindwa ipasavyo ili kila anayekuja arejee nyumbani salama," alisema Mkenyenge huku akiishukuru TAEC na IAEA kwa kuongeza utayari wa nchi.

​Naye mwezeshaji wa mafunzo hayo kutoka Côte d’Ivoire, Lacina Soro, alibainisha kuwa ufanisi wa usalama katika matukio makubwa unategemea ushirikiano kati ya teknolojia na uwezo wa wataalamu, akisisitiza kuwa kuwa na vifaa pekee haitoshi bila uwepo wa mipango madhubuti, tathmini ya vitisho kabla ya tukio, na uratibu mzuri wa mawasiliano kati ya taasisi husika.







Na. Vero Ignatus, Michuzi Tv -Arusha

Naibu Waziri wa Utalii, Hamad Hassan Chande, ametaja uwepo wa utalii wa maombi katika Hifadhi ya Msitu wa Ziwa Duluti, Wilaya ya Arumeru mkoani Arusha,mazingira yake ya asili yana fursa kubwa ya kuendeleza aina mbalimbali za utalii,

Amesema utalii huo ndani ya Hifadhi ya Ziwa hilo unasaidia kukuza imani za watu na kuchangia maendeleo endelevu ya eneo hilo hivyo amewataka wananchi na wadau kuendelea kutunza mazingira na vivutio hivyo kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho kwaajili ya maendeleo ya Kitaifa na kukuza uchumi.

Ametoa rai kwa wawekezaji wa ndani na nje kuchangamkia fursa katika eneo hilo, hususan katika miundombinu na huduma za utalii, ili kuongeza idadi ya watalii na mchango wa eneo hilo kwni Ziwa hilo halikauki na ni sababu kubwa ya kivutio huku akisisitiza Jamii kwa kushirikiana na Serikali pamoja na sekta binafsi katika kulilinda eneo hilo la utalii.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii na Mbunge wa Korogwe Vijijini, Timotheo Mzava, aliwaongoza wajumbe wa Kamati hiyo katika ziara ya kutembelea Hifadhi hiyo kwa lengo la kukagua hali ya uhifadhi, kutathmini fursa za utalii wa ikolojia na kujadili changamoto zinazokabili eneo hilo la Ziwa Duluti

Mzava amepongeza na kuzisihi sekta binafsi kuboresha miundombinu na huduma kuelekea maandalizi ya Tanzania kuwa mwenyeji wa AFCON 2027 ,Sambamba na kuwa taka Watanzania kutembelea vivutio vilivyopo katika Hifadhi hiyo ya msitu wa ziwa Duluti

Peter Myonga ni Mhifadhi Mkuu wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), amesema kuwa TFS imeendelea kuboresha huduma na miundombinu katika Hifadhi ya Msitu wa Ziwa Duluti, ikiwemo kuongeza maeneo ya malazi ili kuhudumia wageni wengi zaidi.

Myonga aliongeza kuwa hifadhi hiyo ina vivutio mbalimbali, ikiwemo utalii wa , matembezi ya kitalii, shughuli za majini,maombi, mandhari ya Mlima Meru , Kilimanjaro,kuna mnyama Kenge, hivyo amewasihi wananchi kutembelea eneo hilo kwa ajili ya kukuza utalii wa ndani.








Timu ya Ushirombo Warriors FC imetwaa ubingwa wa Wilaya ya Bukombe katika mashindano ya KNK CUP 2026, baada ya kuichapa Katome FC mabao 2-0 katika mchezo wa fainali uliochezwa tarehe 7 Septemba 2026 katika Uwanja wa Bukombe Stadium uliopo Mtaa wa Kilimahewa, Kata ya Katente, Tarafa ya Ushirombo, Wilaya ya Bukombe mkoani Geita.

Ushirombo Warriors walionyesha kiwango kizuri na kutumia vyema nafasi walizopata. Bao la kwanza lilifungwa dakika ya 43 na mshambuliaji wao Hames Kigwangala kabla ya mapumziko.

Kama mabingwa, Ushirombo Warriors FC walikabidhiwa kombe, seti tatu za jezi, mipira mitatu pamoja na kitita cha shilingi milioni 5. Katome FC ambao walimaliza nafasi ya pili walikabidhiwa seti mbili za jezi, mipira miwili pamoja na shilingi milioni 3. Nafasi ya tatu ilichukuliwa na Msasa FC ambao walikabidhiwa seti moja ya jezi, mpira mmoja pamoja na shilingi milioni 1.

Zawadi hizo zilikabidhiwa na Mkuu wa Wilaya ya Bukombe, Paskasi Muragili, kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Geita. Mashindano hayo yanafadhiliwa na Mbunge wa Jimbo la Bukombe, Dkt. Doto Biteko.

Mratibu wa Kamati ya Mashindano ya KNK CUP 2026 Wilaya ya Bukombe, Bosco Mwidad, alisema mashindano hayo yameendelea kuwa jukwaa muhimu la kuwaibua vijana wenye vipaji vya soka. Alisema tangu mashindano hayo yalipoanza mwezi Julai mwaka huu, jumla ya timu 248 zilishiriki, huku zawadi zikitolewa kuanzia ngazi ya kata hadi tarafa.

Nahodha wa Ushirombo Warriors FC, Damas Buyenze, alieleza furaha yake baada ya timu hiyo kutwaa ubingwa wa Wilaya kwa mara ya kwanza. Alisema “Nina furaha sana pamoja na wachezaji wenzangu kwa kutwaa ubingwa wa Wilaya, kwani si jambo dogo. Tulijipa moyo, tukajituma na kumsikiliza mwalimu wa timu, na leo tumetwaa ubingwa. Pia namshukuru Mungu kwa kunisaidia kuwa golikipa bora”.

Wananchi wa Bukombe pamoja na wapenda michezo kwa ujumla wamemshukuru Dkt. Doto Mashaka Biteko kwa kuendelea kugharamia mashindano hayo ambayo yamekuwa chachu kubwa ya kukuza na kuibua vipaji vya watoto na vijana katika Wilaya hiyo.











Jumla ya watoto wachanga 15 wenye changamoto ya manjano na watoto zaidi ya 30 njiti hupokelewa kila mwezi katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Geita. Changamoto hizo zimekuwa zikisababisha vifo vingi kwa watoto wachanga.

Hali hiyo imeiibua Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa TAKUKURU Mkoa wa Geita kuona ipo haja ya kuongeza nguvu katika mapambano ya kuwaokoa watoto hao.

TAKUKURU Mkoa wa Geita imetoa vifaa vya kuokoa watoto njiti na wenye manjano, ambavyo ni infant warmer pamoja na photo therapy kwa ajili ya kuzuia vifo vya watoto wachanga.

Akizungumza wakati wa makabidhiano hayo, Naibu Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU Nchini, Neema Mwakalyele amesema zoezi la kukabidhi mashine hizo katika hospitali mbalimbali limefanyika katika zaidi ya mikoa 20 nchini.

Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Geita imepatiwa jumla ya mashine 6 za aina hiyo, wakati mahitaji ni jumla ya mashine 10 ili kumaliza kabisa vifo vya watoto njiti na wenye manjano.

Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mheshimiwa Alexander Pastory Mnyeti, ameishukuru TAKUKURU kwa vifaa hivyo ambavyo vinaenda kuokoa maisha ya watoto wachanga. Amesema atahakikisha anachangia kupatikana kwa mashine zilizobaki ili kumaliza kabisa changamoto hiyo.






- Ushirikiano huu kupitia taasisi zinazosaidia wajasiriamali vyuoni unalenga kuwafikia zaidi ya wajasiriamali 1,000 na kusaidia biashara zaidi ya 40 kukua na kupanuka


Dar es Salaam, Septemba 4, 2026: Vodacom Tanzania Plc leo imetangaza kuingia katika ubia wa miaka mitatu na Bridge for Billions, mtandao wa kimataifa wa ujasiriamali, kwa lengo la kupanua wigo na kuongeza matokeo ya mpango wa Vodacom Digital Accelerator (VDA).

Katika kipindi cha miaka mitatu ya ubia huo, mashirika hayo mawili yatazijengea uwezo na kuziwezesha taasisi zinazosaidia wajasiriamali (ESOs) kote nchini Tanzania na hivyo kuwafikia zaidi ya wajasiriamali 1,000 na kusaidia biashara zaidi ya 40 kukua na kupanuka.

Ushirikiano huu unaashiria mabadiliko katika namna VDA inavyotekeleza na kuongeza matokeo yake. Pamoja na kuendelea na lengo la kusaidia biashara changa moja kwa moja, mpango huu sasa utawekeza pia katika vituo vya kulea na kukuza biashara, vituo vya ujasiriamali, vyuo vikuu na mashirika ya maendeleo ya biashara yanayowasaidia waanzilishi wa biashara kila siku. Hatua hii inalenga kuimarisha mifumo ambayo wajasiriamali nchini Tanzania wanaihitaji hata baada ya kumalizika kwa programu ya kundi fulani la washiriki.

Kupitia makubaliano hayo, Bridge for Billions italeta nchini utaalamu wake katika programu za kulea na kukuza biashara changa (incubation), teknolojia za kidijitali na uzoefu wa kujenga uwezo wa taasisi zinazosaidia wajasiriamali. Taasisi zitakazochaguliwa zitapatiwa mafunzo maalumu, zitawezeshwa kutumia zana na mifumo ya Bridge for Billions, pamoja na kupata msaada katika kubuni programu na kuziendesha.

Aidha, taasisi hizo zitaunganishwa na mtandao wa kimataifa wa washauri na taasisi zinazosaidia wajasiriamali, hivyo kuwawezesha kujifunza, kubadilishana uzoefu na kujenga mahusiano na taasisi nyingine.

Wajasiriamali watakaopatikana kupitia taasisi hizo watapitia mchakato maalumu wa kulea na kukuza biashara zao, huku biashara zitakazoonesha uwezo mkubwa wa kukua zikiendelea kwenye hatua ya acceleration, ambapo zitapatiwa msaada wa kina zaidi katika kukuza biashara na kujiandaa kwa fursa za uwekezaji.

Tangu kuzinduliwa kwake mwaka 2019, Vodacom Digital Accelerator imekuwa ikiunga mkono biashara changa na zinazokua zinazotumia teknolojia kutengeneza bidhaa na huduma zenye uwezo wa kukua, katika sekta mbalimbali ikiwemo afya, kilimo, elimu na huduma za kifedha.

Kupitia awamu mbalimbali, programu hiyo imewapatia wajasiriamali mafunzo, ushauri wa kitaalamu, teknolojia, fursa za kuunganishwa na wawekezaji, pamoja na fursa za kufikia mitandao na washirika wa Vodacom.

Ubia huu wa miaka mitatu unaendeleza safari ya VDA kutoka kwenye programu zinazotekelezwa kwa awamu moja baada ya nyingine hadi kwenye uwekezaji wa muda mrefu katika kuimarisha mfumo wa ujasiriamali nchini.

Kundi la kwanza la taasisi zitakazoshiriki katika mpango huu linatarajiwa kutangazwa Oktoba 2026, huku maombi kwa wajasiriamali yakitarajiwa kufunguliwa mwishoni mwa Septemba 2026.
Mkurugenzi wa Vodacom Business Nguvu Kamando (kushoto), akisalimiana na Mkurugenzi wa Programu za Afrika wa Bridge for Billions, Liliosa Mbirimi (kulia), muda mfupi baada ya kutangazwa kwa ushirikiano wa miaka mitatu kati ya Vodacom Digital Accelerator (VDA) na Bridge for Billions. Ushirikiano huo unalenga kuimarisha mfumo wa ujasiriamali nchini kwa kuwafikia zaidi ya wajasiriamali na wabunifu 1,000 na kusaidia zaidi ya biashara 40 kukua na kupanuka, ushirikiano huu ulitangazwa wakati wa Wiki ya Ubunifu Tanzania (IWTz) 2026, Septemba 3 jijini Dar es Salaam.

Mkurugenzi wa Programu za Afrika wa Bridge for Billions, Liliosa Mbirimi (kulia), akizungumza wakati wa kutangazwa kwa ushirikiano wa miaka mitatu kati ya Vodacom Digital Accelerator (VDA) na kampuni hiyo unaolenga kuimarisha mfumo wa ujasiriamali nchini kwa kuwafikia zaidi ya wajasiriamali na wabunifu 1,000 na kusaidia zaidi ya biashara 40 kukua na kupanuka. Ushirikiano huo ulitangazwa wakati wa Wiki ya Ubunifu Tanzania (IWTz) 2026, Septemba 3 jijini Dar es Salaam. Kushoto ni Mkurugenzi wa Vodacom Business Nguvu Kamando.

Baadhi ya washiriki na wabunifu wakifuatilia uzinduzi wa ushirikiano wa miaka mitatu kati ya Vodacom Digital Accelerator (VDA) na Bridge for Billions unaolenga kuimarisha mfumo wa ujasiriamali nchini uliotangazwa wakati wa Wiki ya Ubunifu Tanzania (IWTz) 2026, Septemba 3 jijini Dar es Salaam.

Mkurugenzi wa Vodacom Business Biashara Nguvu Kamando, akizungumza wakati wa kutangazwa kwa ushirikiano mpya wa miaka mitatu kati ya Vodacom Digital Accelerator (VDA) na Bridge for Billions, unaolenga kuimarisha mfumo wa ujasiriamali nchini na kuwawezesha wajasiriamali na wabunifu kukua. Ushirikiano huo ulitangazwa wakati wa Wiki ya Ubunifu Tanzania (IWTz) 2026, Septemba 3 jijini Dar es Salaam. Kulia ni Mkurugenzi wa Programu za Afrika wa Bridge for Billions, Liliosa Mbirimi.


Mkurugenzi wa Programu za Afrika wa Bridge for Billions, Liliosa Mbirimi (kulia) akifafanua kuhusu ushirikiano mpya wa miaka mitatu kati ya Vodacom Digital Accelerator (VDA) na kampuni hiyo unaolenga kuimarisha mfumo wa ujasiriamali nchini kwa kuwafikia zaidi ya wajasiriamali na wabunifu 1,000 na kusaidia zaidi ya biashara 40 kukua na kupanuka. Ushirikiano huo ulitangazwa wakati wa Wiki ya Ubunifu Tanzania (IWTz) 2026, Septemba 3 jijini Dar es Salaam. Kushoto ni Mkurugenzi wa Vodacom Business Nguvu Kamando.

Top News