Na Mashaka Mhando, Handeni

HATUA ya Serikali ya Awamu ya Sita kuwezesha makundi maalum kiuchumi imeanza kuzaa matunda makubwa Wilayani Handeni, baada ya kikundi cha vijana waliokuwa madereva, makondakta, na wapiga debe eneo la Mkata kufanikiwa kununua gari la abiria aina ya Toyota Coaster.

Mafanikio hayo makubwa yamefikiwa kupitia mkopo wa Shilingi Milioni 90 utokanao na asilimia 10 ya mapato ya ndani ya Halmashauri ya Wilaya ya Handeni kwa mwaka wa fedha 2025/2026.

Taarifa ya mafanikio ya vijana hao imetolewa Leo Augosti 1, mbele ya Wajumbe wa Kamati ya Siasa ya CCM Mkoa wa Tanga, wakiongozwa na Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa (NEC), Bw. Mohammed Salim, waliokuwa katika ziara ya kukagua miradi ya maendeleo wilayani humo.

Akiwasilisha taarifa ya mradi huo unaomilikiwa na kikundi hicho cha vijana cha Mkata, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Handeni, Saitoti Stephen, alisema mradi mzima unagharimu Shilingi Milioni 100. 

Saitoti alifafanua kuwa, kati ya fedha hizo, Shilingi Milioni 10 zilitokana na mtaji wa vijana wenyewe waliokuwa wakijishughulisha na uwakala wa usafirishaji, huku Shilingi Milioni 90 zikiwa ni mkopo usio na riba kutoka halmashauri.

"Kabla ya kuwakabidhi fedha hizi, Halmashauri iliwapeleka vijana hawa kwenye ziara ya kimkakati ya kimafunzo eneo la Chalinze ili kuwajengea uwezo wa kibiashara. Tunafurahi kuona mradi huu sasa unazalisha ajira na kuwawezesha vijana hawa kulea familia zao," alieleza Saitoti.


Rekodi ya Marejesho

Katika hatua inayothibitisha uaminifu na dhamira ya vijana hao, Mkurugenzi huyo alieleza kuwa tayari wameanza kufanya marejesho kulingana na mkataba wao, ambapo mpaka sasa kiasi cha Shilingi Milioni 6.3 kimekwisha rejeshwa serikalini.

Alisema mafanikio hayo na uaminifu ulioonyeshwa umechangiwa kwa kiasi kikubwa na Jukwaa la Vijana la Wilaya ya Handeni, ambalo limekuwa likihamasisha uadilifu, uzalendo, na kutunza amani, sambamba na kuwahamasisha vijana wengine kuchangamkia fursa za kiuchumi.

Mkurugenzi Saitoti alihitimisha kwa kutoa shukrani za dhati kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa uamuzi wake wa makusudi wa kuendelea kutoa mabilioni ya fedha yanayoleta mageuzi ya kiuchumi na kupunguza wimbi la vijana wanaozurura mitaani.



Standard Chartered Foundation, kupitia Standard Chartered Tanzania, imetoa mchango wa TZS 21,456,431.52 kwa ajili ya kuunga mkono Programu ya Mabinti ya CCBRT, ikiwa ni sehemu ya dhamira ya Benki ya kuendelea kukuza ujumuishaji wa kiuchumi na kuongeza fursa kwa makundi yaliyo katika mazingira magumu nchini Tanzania.

Mchango huo utagharamia programu ya wiki sita itakayowanufaisha wanawake 40 kupitia mafunzo ya stadi za kazi, usimamizi wa biashara na elimu ya fedha, pamoja na ununuzi wa mashine za kushona zitakazowawezesha kuanzisha na kuendeleza shughuli za kujiongezea kipato.

Kupitia ufadhili huo, washiriki watapatiwa mafunzo ya ushonaji wa bidhaa za crochet, urembaji wa nguo (embroidery), usimamizi wa biashara na elimu ya fedha. Mafunzo hayo yanalenga kuwajengea wanawake ujuzi wa vitendo na maarifa ya ujasiriamali yatakayowawezesha kujitegemea kiuchumi. Aidha, mashine za kushona zitakazonunuliwa kupitia mchango huo zitawasaidia kuongeza uzalishaji na kipato baada ya kuhitimu mafunzo.

Programu ya Mabinti inayotekelezwa na CCBRT inawalenga wanawake walio katika mazingira magumu, wakiwemo wanawake wenye ulemavu, manusura wa fistula ya uzazi, wasichana walioacha shule na wanawake wanaokabiliwa na changamoto za kiuchumi na kijamii. Kupitia mafunzo ya ujuzi na usaidizi wa ujasiriamali, programu hiyo inawawezesha wanawake kujitegemea kifedha na kuboresha maisha yao.

Ushirikiano huu unaendelea kudhihirisha dhamira ya Standard Chartered ya kuwekeza katika maendeleo ya jamii inazohudumia. Mapema mwaka huu, katika kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Wanawake, wafanyakazi wa Standard Chartered Tanzania walitembelea Kituo cha Mabinti na kukabidhi mashine 12 za kushona pamoja na kutoa mafunzo ya elimu ya fedha kwa wanufaika wa programu hiyo. Hatua hiyo ilionesha dhamira ya Benki ya kuwawezesha wanawake kupitia msaada wa vitendo na kuwajengea uwezo.

Mchango huu pia umetolewa katika mwaka ambao Standard Chartered inaadhimisha miaka 20 ya Mpango wa Kujitolea wa Wafanyakazi, unaotambua mchango wa wafanyakazi wake ambao kwa kipindi cha miongo miwili wamekuwa wakitumia muda, ujuzi na uzoefu wao kuleta mabadiliko chanya katika jamii duniani.

Akizungumza kuhusu mchango huo, Afisa Mtendaji Mkuu na Mkuu wa Kitengo cha Coverage wa Standard Chartered Tanzania, Geofrey Mchangila, alisema:

"Tunajivunia kuendeleza ushirikiano wetu na CCBRT katika kuunga mkono Programu ya Mabinti ambayo imekuwa na mchango mkubwa katika kuwawezesha wanawake. Hii ni mara ya pili kushirikiana na CCBRT. Mapema mwaka huu, wakati wa maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Wanawake, timu yetu ilitembelea kituo hicho, ambapo tulikabidhi mashine 12 za kushona na kutoa mafunzo ya elimu ya fedha kwa wanawake wanaoshiriki katika programu hiyo.

Leo tunaimarisha zaidi dhamira yetu kwa kutoa TZS milioni 21.4 kwa ajili ya kugharamia mafunzo ya stadi za kazi, usimamizi wa biashara na fedha kwa wanawake 40, pamoja na ununuzi wa mashine zaidi za kushona. Tunaamini kuwa programu kama hii zinawapa wanawake ujuzi, maarifa na rasilimali muhimu za kujenga maisha ya kujitegemea na mustakabali wenye fursa zaidi."




Na Mashaka Mhando, Muheza

MJUMBE wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa (NEC), Mohammed Salim 'Ratco', amewataka wasimamizi wa miradi ya maendeleo wilayani Muheza kuhakikisha kunakuwepo na thamani halisi ya fedha (Value for Money) kwenye miradi, ili kumshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa vitendo badala ya maneno.

Ratco ametoa agizo hilo Leo Augosti 1, wakati wa ziara ya Kamati ya Siasa ya CCM Mkoa wa Tanga iliyofanya ukaguzi wa ujenzi wa Kituo cha Afya Misozwe, wilayani humo.

Alisisitiza kuwa, kutokana na Rais Dkt. Samia kutoa mabilioni ya fedha kwa ajili ya kuharakisha maendeleo ya wananchi, kuna kila sababu ya kuhakikisha miradi hiyo inajengwa kwa viwango stahiki na fedha zinatumika kwa makusudio yaliyotarajiwa.

"Tuwe tunamshukuru Rais wetu kwa vitendo, tusimshukuru kwa maneno. Fedha zinazotolewa na Serikali zifanye kazi iliyotarajiwa na kuleta tija kwa wananchi wetu," alisisitiza MNEC huyo.

Katika majumuisho ya ziara hiyo yaliyofanyika eneo la Kwabastola, Ratco alibainisha kuwa ingawa ujenzi wa kituo hicho unaendelea vizuri na umefikia asilimia 68, wasimamizi wanapaswa kuwa makini na kurekebisha mapungufu madogo madogo yaliyoonekana mapema.

Akikazia maelekezo hayo, Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Mkoa wa Tanga, Swaibu Mwanyoka, aliwasihi wasimamizi kuepuka kufanya kazi kimazoea na badala yake wawe waadilifu katika usimamizi wao ili kuepuka hasara.

Awali, akiwasilisha taarifa ya ujenzi huo unaotarajiwa kukamilika ifikapo Oktoba 14, 2026, Mganga Mkuu wa Zahanati ya Misozwe, Rukia Kashegu, alisema mradi huo unagharimu kiasi cha Shilingi Milioni 250.

Rukia alifafanua kuwa mradi huo uliopo Kijiji cha Manyoni, Tarafa ya Ngomeni, unajumuisha jengo la wagonjwa wa nje (OPD), choo cha nje cha wagonjwa, pamoja na miundombinu ya taka za hospitali.

Aliongeza kuwa ujenzi huo ni sehemu ya utekelezaji wa ahadi zilizomo ndani ya Ilani ya CCM ya mwaka 2025/2030, yenye lengo la kuhakikisha wananchi wanakuwa na afya bora itakayowawezesha kushiriki vyema katika shughuli za ujenzi wa taifa.





Jane Mwakyoma,Rukwa.

MAADHIMISHO ya nane nane mwaka 2026 yamefunguliwa leo Aug 1, katika mamlaka ya mji mdogo wa Laela Halmashauri ya wilaya ya Sumbawanga mkoani Rukwa na yatafikia kilele chake Aug 8 mwaka huu,huku maadhimisho hayo yakibeba kauli mbiu ya mwaka huu "Tambua soko,ongeza tija kutekeleza Dira 20250".

Halmashauri hiyo inaadhimisha sikuku hiyo ndani ya wilaya yake kwa kutambua umuhimu wa kilimo kinachotegemewa na wakazi wa wilaya hiyo na Taifa kwa ujumla,ambapo maadhimisho hayo yanaambatana na utoaji wa elimu ya kilimo cha kisasa kwa wananchi,ikiwa maadhimisho hayo kwa mikoa ya nyanda za juu kusini yanaadhimishwa jijini Mbeya.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti wananchi waliofika katika maonyesho hayo,wamepongeza uongozi wa Halmashauri hiyo kwa kuweka maadhimisho ya sikuku ya nane nane ndani ya wilaya yao na kuwa maadhimisho hayo yanatoa frusa kwa wakulima kujifunza mbegu mpya na zenye tija pamoja na kupata elimu ya kilimo cha kisasa na kitakacholeta matokeo chanya kwa wakulima.

Kwa upande wake mkuu wa wilaya ya Sumbawanga Nyakia Chirukile amesema lengo la kuweka maadhimisho hayo katika wilaya hiyo ni kutoa elimu ya kilimo kwa wananchi ili waweze kujifunza matumizi bora ya bembejeo za kilimo zitakazowasaidia wakulima kuinuka kiuchumi.

Aidha amewataka wananchi wa wilaya hiyo kutumia frusa ya maonyesho hayo kupata elimu ya kilimo itakayowasaidia kutoka katika kulima kilimo cha mazoea na kujikita katika kilimo cha kisasa na chenye tija ili kukuza uchumi wao.

Pia ameyataka makampuni yanayosambaza pembejeo za kilimo kutoa elimu sahihi na kuzitolea ufafanuzi mbegu na mbolea zinazofaa katika ukanda huo na kuzingatia utaalamu wa kilimo utakaokuwa na manufaa kwa wakulima wa wilaya hiyo.

Naye Afisa lishe wa Halmashauri ya wilaya ya Sumbawanga Alphani Mwani amesema maonyesho hayo ni muhimu kuendelea kuwepo kila mwaka na wananchi wapate elimu ya kilimo pamoja na elimu ya lishe ili kujenga jamii yenye afya.








Jane Mwakyoma, Aug1,2026, Rukwa.

JESHI la Polisi Wilayani Nkasi mkoani Rukwa limetoa misaada ya mahitaji mbalimbali kwa wazee 30 wasiojiweza ikiwa ni sehemu ya kuimarisha uhusiano kati ya Jeshi la Polisi na jamii pamoja na kuendeleza utamaduni wa kuwajali makundi yenye uhitaji maalumu.

Akizungumza wakati wa kukabidhi misaada hiyo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Rukwa, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi SACP Shadrack Masija amesema Jeshi la Polisi lina wajibu wa kulinda usalama wa raia na mali zao na linaendelea kutekeleza shughuli za kijamii zinazolenga kugusa maisha ya wananchi, hususan wazee wasiojiweza.

Amesema hatua hiyo ni sehemu ya falsafa ya Polisi Jamii inayohimiza ushirikiano, mshikamano na kuwajali wananchi katika nyanja mbalimbali za maisha, huku akitoa wito kwa wadau na jamii kuendelea kuwaunga mkono wazee na makundi mengine yenye mahitaji maalumu.

Kwa niaba ya maafisa wakaguzi na askari wa Wilaya ya Nkasi, Mkuu wa Polisi wa Wilaya hiyo, Wenceslaus Gumha amesema misaada hiyo ni ishara ya upendo na kuthamini mchango wa wazee katika jamii, akibainisha kuwa Jeshi la Polisi litaendelea kushiriki shughuli za kijamii zinazolenga kuimarisha ustawi wa wananchi.

Misaada iliyotolewa imejumuisha blanketi, vitenge, unga, sukari pamoja na mahitaji mengine muhimu ya matumizi ya kila siku ili kuwasaidia wazee hao kukabiliana na changamoto za maisha.

Kwa upande wao, wananchi waliohudhuria hafla hiyo katika viwanja vya Polisi Wilaya ya Nkasi pamoja na wazee walionufaika wamelishukuru Jeshi la Polisi kwa moyo wa kujitolea na kuwajali wenye uhitaji kuwa hatua hiyo imeonyesha kuwa Polisi si walinzi wa usalama pekee bali pia ni wadau wa maendeleo na ustawi wa jamii.







Na Victor Masangu,Kibiti

Mwenyekiti wa Jumuiya ya wazazi Taifa Ndg. Fadhili Maganya ameridhishwa na utekelezaji wa mradi wa maji ambao unatakelezwa na Wakala wa maji na usafi wa mazingira vijijini (RUWASA) Wilaya ya Kibiti ambapo amesema kwamba mradi huo ni mkombozi mkubwa katika kuwahudumia kwa kiasi kikubwa wananchi hao upatikanaji wa maji safi na salama ambapo itawapunguzia adha wanannchi hao kutembea umbari mrefu.

Hayo ameyabainishwa wakati wa ziara yake ya kikazi katika Wilaya ya Kibiti yenye lengo la kuweza kuimarisha chama, kuangalia utekelezaji wa Ilani pamoja na jumuiya zake zote sambamba na kutembelea na kukagua miradi mbali mbali ya maendeleo, ikiwemo sekta ya elimu pamoja na sekta ya maji.

Mwenyekiti huyo amesisitiza kwa uongozi wa Ruwasa kuendelea kuhakikisha wanaweka ulinzi wa kutosha katika mradi huo ambapo amesema chanzo hicho ni muhimu sana kwani ndio tegemezi kubwa la wananchi wa Wilaya ya Kibiti katika suala zima la upatikanaji wa maji safi na salama na kuwahimiza kutunza chanzo cha maji hayo pamoja miundombinu iliyopo.

"Nipende kuchukua nafasi hii kuwapongeza kwa dhati uongozi mzima wa Ruwasa kwa kutekeleza mradi huo wa maji ambao utakuwa ni msaada mkubwa kwa wananchi wa Wilaya ya Kibiti,"amebainisha Mwenyekiti.

Akizungumza katika mkutano wa ndani na wanachama wa chama hicho amewaomba viongozi kuhakikisha kwamba wanatekeleza ilani ya chama kwa vitendo ikiwemo suala la kusimamia fursa za mikopo ya asilimia 10 ambayo inatolewa na Halmashauri.

Pia amewaagiza viongozi wa chama pamoja na madiwani kuhakikisha wanasimamia fedha zinazotolewa kwa ajili ya miradi ya maendeleo.

Meneja huyo amebainisha kwamba lengo kubwa la ukarabati wa mradi huo ni kwa ajili ya kuweza kutatua changamoto ya maji ambazo zinawakabiliwa wananchi wa Wilaya ya Kibiti na kuunga juhudi za serikali ya awamu ya sita katika kuhakikisha ina mtua mama ndoo kichwani

Amebainisha ukarabati wa.mradi wa maji Kibiti mjini umetekelezwa kwa kiasi cha zaidi ya shilingi milioni 312 ambazo fedha hizo zimetolewa na serikali kuu kupitia mfuko wa maji wa fedha Kitaifa (NWF) na kwamba utakuwa ni mkombozi mkubwa katika kutatua changamoto hizo zilizokuwa zinawakabili wananchi.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Kibiti Kanali Joseph Kolombo amempongeza kwa dhati Mwenyekiti wa wazazi Taifa kwa kutekeleza ilani ys chama kwa vitendo ikiwemo suala la kufanya ziara ya kikazi ambayo imekuwa na mafanikio makubwa kutokana na kuweza kukutana na viongozi wa serikali, taasisi wezeshi pamoja na chama.

Kanali Kolombo amebainisha kwamba hali ya amani na utulivu katika Wilaya ya Kibiti inaendelea vizuri na kwamba katika utekelezaji wa ilani wameweza kupokea kiasi cha shilingi milioni 528 kwa ajili ya ujenzi wa shule ya Mchukwi ambapo pia wamepokeai kisi cghha shilingi milioni 700 kwa lengo la kuboresha miundombinu ya barabara hususan zinazowenda maeneo ya Delta na sehemu nyingine.

Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi Taifa ameendelea na ziara yake ya kikazi katika Wilaya ya Kibiti ambapo ameweza kupata fursa ya kuzungumza na wanachama wa CCM, viongozi wa serikali,taasisi wezeshi pamoja na kutembelea baadhi ya miradi mbali mbali ya maendeleo katika sekta ya maji pamoja na elimu.





Mrajis Msaidizi wa Vyama vya Ushirika Mkoa wa Dodoma, Joseph Chitinka, amewataka wakazi wa Dodoma, mikoa jirani na Tanzania kwa ujumla kujitokeza kwa wingi kushiriki maonesho ya kilimo Nanenane yanayoendelea katika viwanja vya Nanenane jijini Dodoma na kutembelea Banda la Kijiji cha Ushirika.

Chitinka amesema Banda hilo limeandaliwa kwa mara ya tatu mfululizo na Tume ya Maendeleo ya Ushirika kwa kushirikiana na Shirikisho la Vyama vya Ushirika TFC kwa lengo la kuonesha bidhaa, shughuli mbalimbali pamoja na huduma zinazotolewa na vyama vya ushirika nchini.

Akizungumza na waandishi wa habari Agosti 1, 2026 katika viwanja vya Nanenane jijini Dodoma, amesema Banda la Kijiji cha Ushirika ni jukwaa maalum linalowakutanisha wadau wa sekta hiyo na kutoa fursa kwa wananchi kufahamu mchango wa vyama vya ushirika katika maendeleo ya kiuchumi.

Amesema kupitia Banda la Mkoa wa Dodoma linaloratibiwa na Chama Kikuu cha Ushirika Mkoa wa Dodoma (DORECU), wananchi wataweza kuona mazao 12 yanayooneshwa, yakiwemo ufuta, choroko na mbaazi.

Aidha, amesema wananchi watapata elimu kuhusu taratibu na sifa za kujiunga na vyama vya ushirika, hususan vya mazao, pamoja na fursa za mikopo zinazopatikana kupitia ushirika.

“Maonesho haya yatasaidia wananchi kufahamu namna vyama vya ushirika vinavyomuinua mkulima, kuongeza kipato na kumsaidia mwananchi kujikwamua kiuchumi,” amesema Chitinka.

Ameongeza kuwa Mkoa wa Dodoma unajivunia mchango wa sekta ya ushirika katika kuchochea maendeleo ya wananchi, huku ukiendelea kusimamia kauli mbiu ya “Linda Ushirika, Chagua Uadilifu.”




Taasisi ya Kuthibiti Ubora wa Mbegu Tanzania (TOSCI) imewataka wakulima nchini kutonunua mbegu yoyote ambayo haina lebo ya utambuzi ya TOSCI, ikieleza kuwa lebo hiyo ndiyo uthibitisho kuwa mbegu imekaguliwa na kuthibitishwa ubora wake.

Wito huo umetolewa na Mkurugenzi Mkuu wa TOSCI, Nyasebwa E. Chimagu, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari katika Maonesho ya Kilimo ya Nanenane yanayofanyika jijini Dodoma Agosti 1, 2026.

Chimagu alisema matumizi ya mbegu bora ni msingi wa kuongeza tija katika uzalishaji wa mazao na kufanikisha malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, amesema kuwa wakulima wanapaswa kuhakikisha mbegu wanazonunua zimefungashwa katika vifungashio rasmi vyenye lebo ya TOSCI.

Alieleza kuwa wakulima wanaweza kuhakiki uhalali wa lebo hiyo kwa kutumia simu za mkononi ili kubaini kama mbegu ni halisi au la, hatua ambayo itawasaidia kuepuka kununua mbegu bandia zinazoweza kusababisha hasara.

Aidha, alisema TOSCI inaendelea kutoa elimu kupitia mabanda yake katika Maonesho ya Kilimo ya Nanenane kuhusu umuhimu wa kutumia mbegu zilizothibitishwa, pamoja na kutoa mafunzo kwa wazalishaji na wafanyabiashara wa mbegu kuhusu taratibu za uzalishaji, usafirishaji na biashara ya mbegu.

Chimagu alibainisha kuwa matumizi ya mbegu bora, sambamba na kuzingatia kanuni bora za kilimo, yanaweza kumwezesha mkulima kuvuna kati ya tani tano hadi kumi kwa hekta.

Aliwahimiza wakulima kutumia Maonesho ya Kilimo ya Nanenane kama fursa ya kupata elimu kuhusu mbegu bora na teknolojia mbalimbali za kilimo zitakazowaongezea tija katika msimu wa kilimo wa mwaka 2026/2027.


Wakala wa Mbegu za Kilimo (ASA) umetangaza mpango wa kuongeza uzalishaji wa mbegu bora hadi kufikia tani 15,000 baada ya mavuno yanayotarajiwa hivi karibuni, hatua inayolenga kuongeza upatikanaji wa mbegu bora kwa wakulima nchini.

Mtendaji Mkuu wa ASA, Mhandisi Innocent C. Masaka , ameyasema hayo Leo Agosti 1, 2026, wakati akizungumza na waandishi wa habari katika Maonesho ya Kilimo ya Nanenane jijini Dodoma ambapo  hadi sasa wakala huo umezalisha tani 7,000 za mbegu, huku ukiendelea kuimarisha uzalishaji kupitia mashamba yake yaliyopo katika kanda mbalimbali za nchi na mahitaji ni kufikia Tani elfu 27.

Amesema ASA katika kuhakikisha wanaongeza uzalishaji wambegu wamejipanga kupanua ushirikiano na sekta binafsi kwa kuwapatia teknolojia za uzalishaji wa mbegu bora ili kuongeza kiwango cha uzalishaji na kuhakikisha wakulima wengi zaidi wanapata mbegu zenye ubora unaohitajika kwa wakati.

Mhandisi Masaka amesema mbegu zinazozalishwa na ASA zimeendelea kuonesha matokeo mazuri katika kanda zote za kilimo nchini, zikiwemo kusini, kaskazini, mashariki na magharibi, huku zikiwa na uwezo wa kuhimili ukame unaotokana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Aidha, amewahimiza wakulima kutumia mbegu bora zilizothibitishwa na TOSCI ili kuongeza tija ya uzalishaji, amesema ASA imeendelea kuimarisha mfumo wa usambazaji kupitia mawakala, wasambazaji wakubwa na Wakala wa Huduma za Ugani Tanzania (NAESA), ambao huwafikishia wakulima teknolojia na mbegu bora kwa wakati.

Amewaalika wananchi kutembelea banda la ASA katika Maonesho ya Nanenane ili kujifunza kuhusu teknolojia za uzalishaji wa mbegu bora na huduma mbalimbali zinazotolewa na wakala huo kabla ya maonesho hayo kuhitimishwa Agosti 8, 2026.







 

Na.Mwandishi wetu

Kampuni ya Mbolea Tanzania (TFC) imeanza utekelezaji wa mpango mkubwa wa kuongeza upatikanaji wa mbolea nchini kwa kuagiza tani 200,000 za mbolea kwa msimu wa kilimo wa mwaka huu, sambamba na uwekezaji katika viwanda vya kuchanganya mbolea na uchakataji wa chokaa ili kuongeza tija ya uzalishaji wa mazao.

Mkurugenzi Mkuu wa TFC, Samuel Ahadi Mshote, amesema hatua hiyo inalenga kuhakikisha wakulima wanapata mbolea bora kwa wakati, kuongeza matumizi ya pembejeo na kuimarisha usalama wa chakula pamoja na uchumi wa kilimo nchini.

Akizungumza leo Agosti 1,2026 kwenye Maonesho ya 49 ya Kilimo ya Nane Nane yanayoendelea kitaifa katika viwanja vya Dkt.John Samuel Malecela jijini Dodoma, Mshote amesema TFC ina jukumu la kuhakikisha upatikanaji wa mbolea zenye ubora unaokidhi mahitaji ya wakulima, huku ikijiandaa kuanza uzalishaji wa mbolea zinazochanganywa kulingana na afya ya udongo na mahitaji ya mazao mbalimbali.

Amesema katika awamu ya kwanza kampuni imeagiza tani 70,000 za mbolea, ambapo tani 35,000 za mbolea aina ya DAP tayari zimewasili nchini na zinafungashwa katika Bandari ya Dar es Salaam kwa ajili ya kusambazwa kwa wakulima kupitia utaratibu wa pembejeo zenye ruzuku ya Serikali.

Aidha, amesema tani nyingine 40,000 za mbolea aina ya Urea zinatarajiwa kuwasili ndani ya muda mfupi ili kuendelea kukidhi mahitaji ya msimu wa kilimo unaoanza.

"Tunataka kuhakikisha hakuna mkulima anayekosa mbolea kwa sababu ya upungufu wa usambazaji. Ndiyo maana tumejipanga kuongeza uagizaji na kuimarisha mtandao wa usambazaji nchini kote," amesema  Mshote.

Amesema TFC imepanua mtandao wake wa huduma kwa kuongeza vituo vya mauzo kutoka nane hadi 26 vilivyopo katika mikoa 22 ya Tanzania Bara, hatua iliyorahisisha wakulima kupata mbolea karibu na maeneo yao.

Mbali na vituo hivyo, kampuni hiyo inashirikiana na zaidi ya mawakala 600 wa pembejeo za kilimo, vyama vya ushirika 29 (AMCOS) pamoja na halmashauri mbalimbali ili kuhakikisha mbolea zinawafikia wakulima hadi ngazi ya vijiji.

Kwa mujibu wa Mshote, tangu TFC ilipoanza kusambaza mbolea mwaka 2022, tayari zaidi ya tani 350,000 za mbolea za ruzuku zimesambazwa kwa wakulima wanaojihusisha na uzalishaji wa mpunga, mahindi, mboga mboga, vitunguu na mazao mengine ya biashara.

Katika hatua nyingine, amesema kampuni hiyo inakamilisha ufungaji wa mtambo wa kisasa wa kuchanganya mbolea katika jiji la Dar es Salaam, ambao utakuwa na uwezo wa kuzalisha tani 300,000 za mbolea kwa mwaka kulingana na mahitaji ya udongo na mazao husika.

Amesema uwekezaji huo utapunguza utegemezi wa uagizaji wa mbolea kutoka nje ya nchi na kuongeza upatikanaji wa mbolea maalumu kwa mazao ya kimkakati kama vitunguu, ufuta, parachichi na mazao mengine yenye thamani kubwa kiuchumi.

Sambamba na hilo,amesema  TFC imeanza kutekeleza mradi wa uchimbaji na uchakataji wa chokaa mkoani Tanga baada ya kupatiwa eneo na Halmashauri ya Jiji la Tanga. Chokaa hicho kitatumika kurekebisha tindikali kwenye udongo pamoja na kuwa malighafi muhimu katika uzalishaji wa mbolea.

Mshote amesema mafanikio ya utekelezaji wa mpango wa ruzuku ya mbolea yameongeza matumizi ya pembejeo nchini kutoka tani 300,000 hadi zaidi ya tani milioni 1.2 kwa mwaka, huku takribani asilimia 80 ya wanufaika wakiwa ni wakulima wadogo.

Amesema ongezeko hilo limechangia kuimarika kwa uzalishaji wa mazao na kuiwezesha Tanzania kufikia kiwango cha zaidi ya asilimia 130 cha kujitosheleza kwa chakula.

Aidha, matumizi ya mbolea kwa hekta yameongezeka kutoka kilo 16 hadi kilo 24, huku Serikali na wadau wa sekta hiyo wakilenga kufikia kiwango cha kilo 30 kwa hekta kama kinavyoelekezwa na Azimio la Abuja kuhusu matumizi ya mbolea barani Afrika.

Amesema utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 unahitaji ushirikiano wa karibu kati ya Serikali, sekta binafsi, taasisi za umma na wananchi ili kuhakikisha malengo yaliyowekwa yanafikiwa kwa wakati na kwa ufanisi.

Ameeleza kuwa dhamira ya Serikali ni kuona Tanzania inafikia uchumi shindani, wenye tija na jumuishi ifikapo mwaka 2050, huku akiahidi kuwa wataendelea kusimamia kwa dhati utekelezaji wa mipango na vipaumbele vilivyowekwa ili kuhakikisha maono hayo yanageuka kuwa matokeo yanayoonekana kwa manufaa ya Watanzania wote.

Mshote amewataka wakulima kutembelea banda la TFC katika Maonesho ya Nane Nane ili kupata elimu kuhusu matumizi sahihi ya mbolea na kufahamu aina zinazofaa kwa mazao na mazingira yao, akisisitiza kuwa matumizi ya pembejeo bora ndiyo msingi wa kuongeza tija, kipato cha mkulima na ukuaji wa sekta ya kilimo nchini.




Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindani (FCC), akizungumza na wadau wakati wa Wiki ya Tisa ya Viwanda ya SADC (SADC Industrialisation Week 2026), inayoadhimishwa katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano (ICC), jijini Durban, Afrika Kusini. Mkutano huo unawakutanisha viongozi wa serikali, sekta binafsi na wadau wa maendeleo kujadili mikakati ya kuharakisha maendeleo ya viwanda na biashara ya kikanda.

DURBAN - AFRIKA KUSINI

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindani (FCC), Bi. Khadija Ngasongwa, amezishauri nchi wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) kuwekeza zaidi katika maendeleo ya viwanda na miundombinu ili kuwawezesha wanawake na vijana kushiriki kikamilifu katika shughuli za uzalishaji.

Bi. Ngasongwa ametoa wito huo jijini Durban, Afrika Kusini, wakati akishiriki Mkutano wa Wiki ya Tisa ya Viwanda ya SADC unaoendelea nchini humo.

"Ushiriki wa FCC katika wiki hii unalenga kuhakikisha sera na miongozo ya ushindani wa haki inazingatiwa katika maendeleo ya viwanda. Tunataka kuona viwanda vya ukanda wetu vinakuwa na ushindani, vinatoa fursa kwa wanawake na vijana, na vinatoa bidhaa zenye ubora kwa walaji," alisema Bi. Ngasongwa.

Ameongeza kuwa uwekezaji katika viwanda vya kuongeza thamani ya malighafi utasaidia kuwainua kiuchumi wanawake na vijana, kupanua masoko ya bidhaa za nchi za SADC na kuongeza mapato ya fedha za kigeni.

Akizungumzia ushiriki wa Tanzania, Bi. Ngasongwa amesema mkutano huo unaendana na vipaumbele vya maendeleo ya Tanzania hususan katika sekta za madini, kilimo, bidhaa za afya, miundombinu na ubunifu.

"Ushiriki wa Tanzania una umuhimu mkubwa kwa sababu unajikita katika kuimarisha mnyororo wa thamani. Ni maeneo muhimu katika safari ya Tanzania kuelekea uchumi wa viwanda na kufikia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050," alisema.

Bi. Ngasongwa pia amewataka wadau wa fedha waliopo katika mkutano huo ikiwemo TIB, Exim Bank, BADEA na Nedbank kushirikiana katika kuhamasisha upatikanaji wa mitaji kwa ajili ya miradi ya maendeleo na uwekezaji nchini.

Amehitimisha kwa kusema kuwa Tanzania imebarikiwa kuwa na madini ya kimkakati na rasilimali nyingine. Hivyo ni muhimu kuyachakata ndani ya nchi badala ya kuuza malighafi ili kuongeza thamani, kuzalisha ajira na kuchochea ukuaji wa viwanda.

Mkutano wa Wiki ya Viwanda ya SADC ulifunguliwa rasmi Julai 27, 2026 na ulihitimishwa Julai 31, 2026 na umetoka na maazimio ya kuimarisha ushirikiano wa kikanda katika biashara, uwekezaji na maendeleo ya viwanda kama sehemu ya maandalizi ya Mkutano wa 46 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa SADC utakaofanyika tarehe 17 Agosti, 2026 Jijini Durban, Afrika Kusini.





Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindani (FCC), akizungumza na wadau wakati wa Wiki ya Tisa ya Viwanda ya SADC (SADC Industrialisation Week 2026), inayoadhimishwa katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano (ICC), jijini Durban, Afrika Kusini. Mkutano huo unawakutanisha viongozi wa serikali, sekta binafsi na wadau wa maendeleo kujadili mikakati ya kuharakisha maendeleo ya viwanda na biashara ya kikanda.



Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindani (FCC), Bi. Khadija Ngasongwa (katikati), akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya washiriki kutoka Tanzania wakati wa Mkutano wa 9 wa Wiki ya Viwanda wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC Industrialisation Week), unaofanyika jijini Durban, Afrika Kusini.



Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Mahusiano kwa Umma, Bi. Roberta Feruzi akitoa maelezo kuhusu huduma zinazotolewa na FCC kwa baadhi ya wadau waliotembelea Banda la Tanzania, pembezoni mwa Mkutano wa Wiki ya Viwanda ya SADC (SADC Industrialisation Week 2026) unaofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano (ICC), jijini Durban, Afrika Kusini.

Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba ameipongeza Benki ya NMB kwa kuendelea kusogeza huduma za kifedha karibu na wananchi kupitia matumizi ya teknolojia na mkakati wa Rural Banking, akisema Serikali itaendelea kuboresha mazingira ya biashara na kupunguza gharama za miamala ya kifedha.

Akimkaribisha Waziri Mkuu katika banda la NMB kwenye Maonesho ya Nanenane, Mkuu wa Idara ya Biashara za Serikali wa benki hiyo, Bi. Vicky Bishubo, alisema NMB imeendelea kuwekeza katika sekta ya kilimo, uvuvi na ufugaji, ikiwa tayari imetoa mikopo yenye thamani ya Sh. trilioni 2.3 kwa sekta hizo.

Alisema benki hiyo pia imewawezesha vijana kupata mikopo ya hadi Sh. milioni mbili kupitia teknolojia bila dhamana wala kwenda tawi, huku huduma za Rural Banking zikiendelea kufika katika masoko na minada ya biashara na mifugo katika maeneo mbalimbali nchini.

Mbali na huduma za kifedha, NMB inaendelea kutoa elimu ya fedha kupitia NMB Kijiji Day na kushirikiana na vyuo vikuu kuwajengea vijana ujuzi unaohitajika katika uchumi unaotegemea teknolojia na ubunifu.

Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba (kushoto) akisikiliza maelezo kutoka kwa Mkuu wa Idara ya Biashara za Serikali wa Benki ya NMB, Bi. Vicky Bishubo, alipotembelea banda la benki hiyo katika Maonesho ya Kitaifa ya Kilimo Nanenane yanayoendelea kwenye Viwanja vya John S. Malecela, Nzuguni mkoani Dodoma jana. NMB ni mdhamini wa maonesho hayo.







Top News