Na Belinda Joseph-Tanga.

Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea Tanzania (TFRA) Kanda ya Kaskazini imetumia Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu jijini Tanga kuelimisha wananchi kuhusu matumizi sahihi ya mbolea, ubunifu wa kiteknolojia pamoja na fursa za mbolea ya ruzuku kwa wakulima.

Akizungumza na Michuzi Tv Agosti 18, 2026 katika viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara jijini Tanga, Meneja wa TFRA Kanda ya Kaskazini, Gothard Liampawe, amesema TFRA imejipanga kutumia mashamba ya mfano kuwafundisha wakulima matumizi sahihi ya mbolea ili kuongeza uelewa na tija katika uzalishaji.

Amesema pamoja na elimu kupitia mashamba ya mfano, TFRA imebuni mifumo mbalimbali ya kiteknolojia inayorahisisha utekelezaji wa majukumu yake, ikiwemo Mfumo wa FIS, unaomwezesha mfanyabiashara kujisajili na kuomba leseni ya biashara, kusajili mbolea na kupata vibali vya kusafirisha au kuingiza mbolea nchini bila kufika katika ofisi za TFRA.

“Mfanyabiashara anaweza kutumia kompyuta yake akiwa mahali popote alipo kufanya maombi hayo bila kulazimika kufika ofisini, hivyo tunaokoa muda na gharama za usafiri,” amesema Liampawe.

Amesema ubunifu huo umeipa TFRA fursa ya kushiriki katika Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu jijini Tanga, kwa lengo la kuwaonesha Watanzania hatua iliyofikiwa katika matumizi ya teknolojia na namna inavyoweza kurahisisha huduma mbalimbali.

Liampawe amesema kuelekea msimu mpya wa kilimo, TFRA Kanda ya Kaskazini imejipanga kuimarisha huduma kwa wakulima na watoa huduma katika sekta ya mbolea kwa kuwatembelea wadau na kuhakikisha wanapata huduma bora, huku ikipanua wigo wa elimu kupitia kampeni ya “Mali Shambani, Silaha Mbolea.”

Amesema katika mwaka wa 2025/2026, Kanda ya Kaskazini imesimamia utekelezaji wa mpango wa mbolea za ruzuku ambapo zaidi ya wakulima 650,000 wamejisajili na kuwa tayari kunufaika na mpango huo, huku wakulima 173,000 tayari wakiwa wamenufaika na jumla ya tani 179,000 za mbolea hadi wiki iliyopita.

Ameutaja mkoa wa Kilimanjaro kuwa kinara kwa matumizi ya mbolea za ruzuku katika Kanda ya Kaskazini, ukifuatiwa na Arusha, Manyara na Tanga, huku zaidi ya Shilingi bilioni 80 zikiwa zimetumika katika upatikanaji wa mbolea hizo.

Aidha, Liampawe amewahimiza wakulima ambao tayari wamejisajili kutotumia vibaya fursa hiyo ya ruzuku inayotolewa na Serikali, huku ambao hawajajisajili akiwataka kufanya hivyo ili waweze kunufaika na mpango huo na kuongeza tija katika kilimo.




Na Belinda Joseph-Tanga

Serikali imeanza mchakato wa kutafuta eneo kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha uhakiki wa malori ya mafuta katika Mkoa wa Tanga, hatua inayolenga kuwaondolea wafanyabiashara usumbufu, muda na gharama za kusafiri hadi Mkoa wa Pwani kupata huduma hiyo.

Hayo yameelezwa na Meneja wa Wakala wa Vipimo (WMA) Mkoa wa Tanga, Julius Temba, leo Agosti 18, 2026, wakati akizungumza katika mwendelezo wa Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu inayoendelea jijini Tanga.

Temba amesema mchakato huo umeanza katika mwaka wa fedha 2026/2027 baada ya Serikali kutambua changamoto inayowakabili wafanyabiashara wa malori ya mafuta wanaohitaji huduma ya uhakiki.

Amesema kwa sasa, wafanyabiashara kutoka Tanga hulazimika kusafiri hadi eneo la Misugusugu, Mkoa wa Pwani, kwa ajili ya kuhakiki malori yao, hali inayoongeza gharama na muda wa kupata huduma hiyo.

Amesema kituo hicho kinatarajiwa kujengwa katika eneo litakalokuwa kwenye barabara ya Segera kuelekea Tanga, na kikikamilika kitasaidia kurahisisha huduma ya uhakiki wa malori ya mafuta kwa wafanyabiashara wa Tanga na maeneo jirani.

Amesema bado kuna changamoto ya baadhi ya watu kutumia vipimo visivyo sahihi, hivyo Wakala unaendelea kutoa elimu na kuimarisha ufuatiliaji ili kuhakikisha wananchi wanatumia vipimo vinavyokidhi viwango vinavyotakiwa.

Amesema kupitia maonesho hayo, WMA inalenga kuwafikia wananchi wengi zaidi na kuwaelimisha kuhusu umuhimu wa vipimo sahihi, huku ikiendelea kushirikiana na Serikali katika kuboresha huduma za vipimo mkoani Tanga.






Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiongoza Ujumbe wa Tanzania kwenye mazungumzo Rasmi na Ujumbe wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) ulioongozwa na Rais wa Nchi hiyo, Mhe. Félix Antoine Tshisekedi Tshilombo katika Ikulu Ndogo ya Zanzibar, tarehe 18 Agosti, 2026.


 


New Delhi, India — 18 Agosti 2026

Mtaalamu wa Tiba Asili na Katibu Mkuu wa Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira Tanzania (TRAMEPRO), Boniventura F. Mwalongo, akiwa New Delhi, India, ameunga mkono wito wa Chifu Felix G. L. Mfunda wa Jamii ya Wandondi na Wandwewe wa kuwaombea waliotangulia mbele ya haki pamoja na kuiombea Tanzania, Afrika na dunia kwa ujumla.

Mwalongo amesema wito huo una umuhimu mkubwa katika kipindi ambacho jamii zinahitaji kuimarisha mshikamano, maelewano, amani, haki na maendeleo ya pamoja.

Ametoa wito kwa viongozi wa Serikali, viongozi wa dini na kimila, vijana, wanawake, wazee, wasomi, wataalamu, wafanyabiashara, wajasiriamali, mashirika ya kiraia na vyombo vya habari kushirikiana katika juhudi zinazolenga kujenga jamii yenye amani, utulivu na ustawi.

Amani Yaenda Sambamba na Kulinda Mazingira

Katika taarifa yake, Mwalongo amesisitiza kuwa amani haipaswi kutazamwa katika mahusiano ya binadamu pekee, bali inapaswa pia kuhusisha heshima kwa uhai wa viumbe na mazingira yanayowezesha maisha.

Amesema maji, udongo, hewa na joto ni sehemu muhimu za mifumo ya mazingira inayowezesha uhai, hivyo kulinda vyanzo vya maji, ardhi, misitu na bayoanuai ni jukumu la pamoja la kizazi cha sasa kwa manufaa ya vizazi vijavyo.

Kwa mtazamo huo, amesema wito wa amani unapaswa pia kuwa fursa ya kutafakari uhusiano uliopo kati ya utu, afya, mazingira, haki na maendeleo.

Wito kwa Vijana

Mwalongo amewataka vijana kutumia nguvu, vipaji na maarifa yao katika elimu, teknolojia, ubunifu, ujasiriamali, sanaa, michezo na utunzaji wa mazingira.

Amesisitiza umuhimu wa vijana kukataa kutumiwa katika chuki, migawanyiko na vurugu, badala yake washiriki katika kujenga jamii yenye fursa na maendeleo.

Aidha, amezialika familia, jumuiya za kidini na kimila, taasisi za kiraia, wataalamu, wafanyabiashara, wasanii, wanamichezo na wadau wengine wa maendeleo kushirikiana katika kujenga jamii yenye utulivu na ustawi.

Amesema tofauti za imani, mila, maeneo au mitazamo hazipaswi kuwa kikwazo cha kushirikiana katika mambo ya msingi yanayowahusu watu wote, ikiwemo uhai, utu, haki, amani na maendeleo.

Kuwakumbuka Waliotangulia, Kuwalinda Walio Hai

Mwalongo amesema dhamira ya Chifu Felix G. L. Mfunda ya kuwaombea waliotangulia mbele ya haki inatoa nafasi ya kutafakari thamani ya maisha na wajibu wa kizazi cha sasa.

Amesema jamii inapaswa kuwakumbuka waliotangulia kwa heshima, kuwalinda walio hai kwa utu, kuheshimu uhai wa viumbe wengine na kutunza mazingira yanayoshirikishwa na viumbe vyote.

Wito wa Pamoja kwa Tanzania, Afrika na Dunia

Akihitimisha taarifa yake, Mwalongo ametoa pongezi kwa Chifu Felix G. L. Mfunda na Jamii ya Wandondi na Wandwewe kwa dhamira ya kuunganisha tafakuri, maombi, utu, mazingira na wajibu wa pamoja katika kujenga Tanzania, Afrika na dunia yenye amani na maendeleo.

Ametoa wito kwa viongozi na makundi yote ya jamii kuunga mkono juhudi zinazolenga kuimarisha maelewano, kulinda uhai na kutengeneza mazingira bora kwa maendeleo ya wote.

“Tuiombee Tanzania. Tuiombee Afrika. Tuiombee dunia nzima. Tuwakumbuke waliotangulia. Tuwalinde walio hai. Tuheshimu uhai wa viumbe vyote na tulinde mazingira kwa ajili ya vizazi vijavyo,” amesema Mwalongo.

Amehitimisha kwa dua: “Mungu awarehemu waliotangulia mbele ya haki. Mungu ailinde Tanzania, aibariki Afrika na alete amani duniani.”

Imetolewa New Delhi, India, tarehe 18 Agosti 2026.

BONIVENTURA F. MWALONGO  Katibu Mkuu Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira Tanzania (TRAMEPRO)

Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ampokea Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) Mhe. Félix Antoine Tshisekedi Tshilombo, Ikulu Ndogo ya Zanzibar.





 

Na Mwandishi Wetu.

Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Queen Sendiga, amezindua rasmi vifaa maalum (KIT) vitakavyotumiwa na washiriki wa Manyara Tanzanite Marathon 2026, huku idadi ya watu waliojiandikisha kushiriki mbio hizo za hisani ikifikia 2,200.

Uzinduzi wa KIT hiyo, inayojumuisha T-shirt, kofia na namba za washiriki, umefanyika Agosti 17, 2026, mjini Babati, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya mwisho kuelekea mbio hizo zinazotarajiwa kufanyika Agosti 22, 2026.

Manyara Tanzanite Marathon 2026 imeandaliwa ikiwa na lengo la kuchangisha fedha zitakazosaidia kuboresha huduma za afya kwa watoto njiti katika Mkoa wa Manyara, hususan katika maeneo yanayohitaji miundombinu na huduma bora zaidi kwa watoto wanaozaliwa kabla ya muda.

Kaulimbiu ya mbio hizo mwaka huu ni “Hatua Moja, Okoa Maisha ya Mtoto,” inayolenga kuhamasisha wananchi, taasisi, kampuni na wadau mbalimbali kushiriki katika tukio hilo huku wakitoa mchango wa moja kwa moja katika kuboresha maisha ya watoto njiti.

Akizungumza katika uzinduzi huo, RC Sendiga amehimiza wananchi na wadau mbalimbali kuendelea kujitokeza kwa wingi kushiriki mbio hizo, akieleza kuwa mwitikio wa watu 2,200 waliojisajili hadi sasa ni ishara ya namna jamii inavyoguswa na ajenda ya kuboresha afya na ustawi wa watoto.

Idadi hiyo ya washiriki inatarajiwa kuongezeka kadri siku ya mbio inavyokaribia, huku waandaaji wakiendelea kutoa wito kwa watu ambao bado hawajajisajili kutumia fursa hiyo kushiriki katika tukio lenye lengo la kuchangia ustawi wa watoto na maendeleo ya afya mkoani Manyara.

Mbali na kushiriki katika mbio hizo, tukio hilo limeandaliwa pia kwa namna inayolenga kukuza utalii wa ndani na kuifanya Manyara kuwa sehemu ya kuvutia kwa wageni kutoka ndani na nje ya Tanzania. Washiriki watakaokuwa wamechagua kifurushi kinachojumuisha ziara ya utalii watapata fursa ya kutembelea Hifadhi ya Taifa ya Tarangire baada ya kumalizika kwa mbio.

Uhusiano kati ya mbio hizo na utalii unalenga kuwapa washiriki uzoefu mpana zaidi, huku ukiendelea kutangaza vivutio vya utalii vilivyopo mkoani Manyara na kuchochea shughuli za kiuchumi zinazotokana na utalii.

Manyara Tanzanite Marathon imeendelea kujijenga kama moja ya matukio yanayounganisha michezo, afya, utalii na uwajibikaji kwa jamii. Kupitia mbio hizo, waandaaji wanatarajia kuhamasisha watu kutoka makundi mbalimbali kushiriki katika jitihada za kuchangia huduma za afya kwa watoto njiti.

Kwa mwaka 2026, msisitizo umewekwa katika kaulimbiu “Hatua Moja, Okoa Maisha ya Mtoto,” huku fedha zitakazopatikana kupitia mbio hizo zikilenga kusaidia ujenzi na uboreshaji wa huduma kwa watoto njiti katika Mkoa wa Manyara.

Uzinduzi wa KIT hiyo umeongeza hamasa kuelekea Agosti 22, ambapo Babati inatarajiwa kuwa kitovu cha tukio hilo litakalowakutanisha washiriki, wadau wa afya, taasisi, wafanyabiashara, watalii na wananchi kwa ujumla katika hatua ya pamoja ya kuokoa maisha ya watoto njiti.


WADAU wa Forodha wakiwemo Mawakala wa Forodha na Maafisa Forodha Mkoa wa Kigoma wamejengewa uwezo kuhusiana na mabadiliko yaliyofanywa na Serikali kupitia Sheria ya Fedha ya mwaka 2026 pamoja na taratibu Forodha.

Elimu hiyo imelenga kuwawezesha
Wadau wa Forodha kuwa na uelewa wa pamoja juu ya Sheria, kanuni na taratibu za forodha na kuwawezesha kutimiza majukumu yao kwa ufanisi na kulipa kodi za Serikali kwa usahihi ili kurahisisha ufanyaji wa biashara na kukuza uchumi nchini.

Elimu hiyo imetolewa na Allan Maduhu, Afisa Forodha Mkuu na Hassan Minga, Afisa Mfawidhi Forodha-Dodoma ambao wamewataka wadau wa Forodha kufuata sheria na taratibu ili kuwawezesha kutekeleza sheria mpya ya Fedha ya mwaka 2026 ikiwemo kufahamu misamaha mbalimbali iliyotolewa na serikali kwa lengo la kuchochea sekta za uzalishaji pamoja na ukuaji wa viwanda nchini.

Misamaha iliyotolewa ni pamoja na msamaha wa Kodi ya Ongezeko la Thamani kwenye nyuzi za kutengenezea nyavu za uvuvi, nyavu za uvuvi zilizozalishwa na wazalishaji wa nyavu za uvuvi nchini pamoja na vifungashio vya maziwa kwa ajili ya kuchochea sekta ya maziwa nchini.

Aidha, Kaimu Meneja Msaidizi wa Forodha Mkoa wa Kigoma Mohamed Mnonda, amesema kulingana na shughuli za Forodha wamejipanga kutekeleza Sheria ya Fedha 2026 ili kuongeza uwajibikaji na ufanisi wa kiutendaji ili kuwezesha na kuboresha ufanyaji wa Biashara mkoani Kigoma.

Kwa upande wa Mawakala wa Forodha wakiongozwa na Dunia Salutwe, wameahidi kufuata sheria na taratibu za Forodha na kuhakikisha wateja wao ambao ni waagizaji na wasafirishaji nje wa bidhaa wanalipa kodi stahiki.


Na Mwandishi Wetu


SERIKALI imedhamiria kuendelea kuimarisha afua za masuala ya UKIMWI nchini kwa kuboresha mazingira ya utekelezaji wa shughuli hizo, huku ikihimiza ushirikiano na wadau mbalimbali katika kuendeleza mapambano dhidi ya UKIMWI.

Kauli hiyo imetolewa na Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Dkt. Jim Yonazi, alipotembelea na kujionea utekelezaji wa shughuli zinazotekelezwa na vikundi vya watu wanaoishi na Maambukuzi ya Virusi vya UKIMWI katika Wilaya ya Nyamagana, Jijini Mwanza.

Akiwa katika ziara hiyo, Dkt. Yonazi amesema Serikali imeendelea kuboresha mazingira na kutenga bajeti inayosaidia kuratibu na kutekeleza afua za masuala ya UKIMWI nchini, huku ikishirikiana na wadau mbalimbali

“Ushirikiano ni muhimu sana kwani, tunaamini unauwezo wa kutuvusha katika mapambano dhidi ya VVU, ambapo tumeendelea kuunganisha nguvu pamoja katika mapambano hayo,” alisema Dkt. Yonazi.

Aliongeza kuwa Ofisi ya Waziri Mkuu, yenye dhamana ya kuratibu shughuli zote za Serikali, ikiwemo masuala ya UKIMWI, itaendelea kuhakikisha vifaa na huduma zinatolewa kwa wakati na ubora kwa WAVIU, huku kanuni na taratibu za afya zikizingatiwa.

Dkt. Yonazi Ametumia jukwaa hilo kuiasa jamii kuendelea kupima afya ili kujitambua na kuchukua hatua za mapema endapo mtu atabainika kuwa na maambukizi ya VVU, ili aweze kuishi kwa tahadhari na kuwalinda wengine.

Kwa upande wake Katibu Tawala Mkoa wa Mwanza, Ndugu Balandya Elikana, amesema kuwa mkoa umechukuwa hatua madhubuti kuimarisha mapambano dhidi ya UKIMWI kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa sekta ya afya na kamati za utekelezaji wa mikakati ya kuzuia maambukizi, huku wakihimiza upatikanaji wa huduma bora na elimu kwa jamii.

“Jamii inaendelea kuhamasishwa kuhusu upimaji wa afya kwa hiari na matumizi sahihi ya njia za kujikinga na maambukizi ya Virusi vya UKIMWI pamoja na kuendelea kushirikiana kwa karibu na mashirika na wadau wa afya ili kuboresha huduma za kinga na tiba,” alisema Elikana

Naye Mganga Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Dkt. Kheri Kagya, akiwasilisha taarifa ya hali ya UKIMWI mkoani humo, amesema Mkoa wa Mwanza una kiwango cha maambukizi ya VVU cha asilimia 4.7, ikilinganishwa na kiwango cha kitaifa cha asilimia 4.4, kwa mujibu wa matokeo ya Utafiti wa Kitaifa wa THIS 2022/2023.

Alisema kwa mujibu wa taarifa ya DHIS2 Annual Report ya mwaka 2025/2026, Mkoa wa Mwanza unakadiriwa kuwa na idadi ya watu wanaoishi na VVU (WAVIU) 112,685.

“Mkoa, kwa kushirikiana na wadau, umeendelea kutoa elimu ya kujikinga dhidi ya maambukizi ya VVU kwa kuhamasisha matumizi sahihi ya kondomu. Katika kipindi cha mwaka 2025/2026, Mkoa ulisambaza jumla ya kondomu 2,265,772 katika jamii, hususani sehemu za kulala wageni, sehemu za kuuzia vileo (baa), kumbi za starehe na kwenye mikusanyiko mbalimbali,” alisema.






Harambee ya kuchangisha fedha na vifaa kwa ajili ya kuendeleza ujenzi wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Kaskazini, Jimbo la Kilimanjaro, kupitia Usharika wa Msitu wa Tembo, Mtaa wa Israel, imefanyika kwa mafanikio huku viongozi na wadau mbalimbali wakijitokeza kuunga mkono ujenzi huo.

Katika harambee hiyo, Mdau wa maendeleo wilayani Simanjiro, Taiko Ole Kulunju, ameendelea kuonesha mshikamano wake katika kusaidia shughuli za maendeleo kwa kuchangia kiasi cha shilingi milioni 4 pamoja na mifuko 100 ya saruji, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuhakikisha ujenzi wa jengo hilo unakamilika.

Taiko Ole Kulunju amesema mchango wake ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za waumini na uongozi wa kanisa katika kuhakikisha wanapata jengo lenye mazingira bora kwa ajili ya ibada pamoja na shughuli mbalimbali za kijamii.

Amesisitiza kuwa maendeleo hayawezi kufikiwa na mtu mmoja pekee, bali yanahitaji ushirikiano wa viongozi, taasisi za dini, wafanyabiashara, wadau wa maendeleo na wananchi kwa ujumla, bila kujali tofauti zao.

Harambee hiyo pia imehudhuriwa na viongozi mbalimbali wa serikali, akiwemo Frank Ole Leshwa, mwakilishi wa Mbunge wa Jimbo la Simanjiro, Mhe. James Ole Milya, pamoja na madiwani mbalimbali kutoka Wilaya ya Simanjiro. Kwa pamoja, viongozi hao wamechangia zaidi ya shilingi milioni 21, ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za waumini katika kukamilisha ujenzi wa kanisa hilo.

Kwa upande wake, Diwani mwenyeji na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro, Mh Kaleya Mollel, ambaye alikuwa mgeni rasmi katika harambee hiyo, amewashukuru viongozi, waumini na wadau wote waliojitokeza kuchangia ujenzi huo kwa fedha, vifaa na namna nyingine mbalimbali.

Mhe. Kaleya amesema ushirikiano na moyo wa kujitolea uliooneshwa na washiriki wa harambee hiyo ni mfano mzuri wa mshikamano unaopaswa kuendelezwa katika jamii, hususan katika kusaidia miradi yenye manufaa kwa wananchi.

Lengo la harambee hiyo ni kuchangisha fedha na vifaa kwa ajili ya kuendeleza ujenzi wa jengo la kanisa, ikiwemo kukamilisha hatua mbalimbali za ujenzi kutoka kwenye lenta ya kwanza na ya pili hadi hatua ya upauaji, pamoja na mahitaji mengine muhimu.

Mchango wa Taiko Ole Kulunju na viongozi wengine katika harambee hii unaonesha kuwa maendeleo ya jamii hayapaswi kubaki kuwa jukumu la taasisi au kundi moja pekee. 

Pale viongozi, taasisi za dini, wafanyabiashara na wananchi wanapoweka tofauti zao pembeni na kuungana kwa lengo moja, miradi ya kijamii hupata nguvu na kasi ya kukamilika. 

Harambee hii ni mfano unaothibitisha kuwa mshikamano, kujitolea na uwajibikaji wa pamoja vinaweza kuwa chachu ya maendeleo endelevu katika jamii.




 Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba Nchini (TMDA), imeingia mashirikiano na Mamlaka ya Udhibiti wa Dawa ya Denmark, (Danish Medicines Agency 

-DKMA) katika nyanja ya udhibiti wa bidhaa tiba Nchini.

Hayo yamebainishwa wakati wa kikao maalum kilichofanyika Jijini Arusha hivi karibuni, ambapo ujumbe wa DKMA umekutana na uongozi wa TMDA ulioongozwa na Mkurugenzi Mkuu wake Dkt. Adam Fimbo.

Katika kikao hicho, maeneo ya ushirikiano yaliyojadiliwa ni pamoja na matumizi ya Teknolojia ya Akili Unde 'AI' katika udhibiti wa vifaa tiba, ufuatiliaji wa ubora na usalama wa bidhaa tiba pamoja na usugu wa vimelea vya magonjwa dhidi ya dawa.

Wakizungumza baada ya kikao hicho, pande zote mbili zimesema ushirikiano huo utasaidia kubadilishana uzoefu, taarifa za kisayansi na kuimarisha mifumo ya udhibiti ili kuhakikisha bidhaa tiba zinazopatikana ni salama, zenye ubora na zinafaa.

Aidha, TMDA ni miongoni mwa mamlaka bora barani Afrika katika ubora wa maabara. Maabara yake imepata hadhi ya WHO Prequalified na ipo katika orodha ya maabara 57 duniani zilizothibitishwa na WHO.

Kwa upande wa DKMA ina dhamira ya kuwa kinara katika ushirikiano wa kitaifa na kimataifa na mamlaka za dawa duniani kote.






 


Na Oscar Assenga, Tanga



WAZIRI wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda, anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika uzinduzi wa Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu 2026, inayofanyika katika Viwanja vya Usagara, jijini Tanga.

Maonyesho hayo yaliyoanza Agosti 15 na yanatarajiwa kuendelea hadi Agosti 24, mwaka huu, yanalenga kuonyesha mchango wa elimu, ujuzi, sayansi, teknolojia na ubunifu katika kufikia malengo ya maendeleo ya Taifa kupitia Dira ya Taifa 2050.

Akizungumza kuhusu maandalizi ya maonyesho hayo, Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Balozi Dk Batilda Burian, alisema mkoa huo umejiandaa kikamilifu kumpokea Profesa Mkenda pamoja na washiriki wengine watakaohudhuria tukio hilo.

Dk Batilda alisema Serikali ya Mkoa imeimarisha maandalizi, ikiwemo ulinzi na usalama, ili kuhakikisha washiriki na wananchi wanaotembelea maonyesho hayo wanapata mazingira salama na rafiki.

“Tanga inajivunia kuwa mwenyeji wa maonyesho haya. Tunawahakikishia Wizara ya Elimu na wananchi kuwa Serikali ya Mkoa imejipanga kuhakikisha ulinzi na usalama unaimarishwa wakati wote wa maonyesho,” alisema.

Alisema maonyesho hayo ni fursa muhimu kwa wananchi kujionea kwa vitendo namna Serikali, taasisi za elimu, watafiti na wabunifu wanavyoshiriki katika kuleta maendeleo ya Taifa.

Kaulimbiu ya maonyesho hayo ni “Elimu, Ujuzi na Ubunifu: Njia ya Kufikia Dira ya Taifa 2050,” ambayo, kwa mujibu wa Dk Batilda, inaendana na hatua ambayo Taifa limefikia katika utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050.

Alisema kila sekta, taasisi, wizara, mkoa na halmashauri ina wajibu wa kuwaelimisha wananchi kuhusu Dira ya Taifa 2050 na nafasi yao katika kuifikia.

“Maonyesho haya yataonyesha Tanzania tunayotaka kuifikia ifikapo mwaka 2050. Taasisi za elimu, vyuo vya ufundi, taasisi za utafiti na shule zitaonyesha mchango wao katika kufikia dira hiyo,” alisema.
Washiriki zaidi ya 300

Dk Batilda alisema zaidi ya washiriki 300 kutoka maeneo mbalimbali wanashiriki katika maonyesho hayo, wakiwemo wawakilishi kutoka vyuo vikuu, taasisi za utafiti na maendeleo, vyuo vya mafunzo na ufundi stadi pamoja na taasisi binafsi zinazohusiana na sayansi na teknolojia.

Alisema washiriki hao watapata fursa ya kuonyesha bunifu, teknolojia, ujuzi na shughuli mbalimbali zinazohusiana na elimu na maendeleo ya Taifa.

Aidha, alisema maonyesho hayo yanatoa fursa muhimu kwa vijana wanaotarajia kujiunga na vyuo vikuu na taasisi nyingine za elimu kupata taarifa sahihi kuhusu fursa za elimu na namna ya kufanya maombi ya kujiunga na vyuo.

“Vijana wanaoanza mchakato wa kujiunga na vyuo vikuu Mtapata fursa ya kuelekezwa namna sahihi ya kujaza maombi na kupata taarifa nyingine muhimu kuhusu elimu ya juu,” alisema.
Sh156 bilioni elimu Tanga

Katika hatua nyingine, Dk Batilda alimshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa uwekezaji mkubwa unaofanywa katika sekta ya elimu, akisema Mkoa wa Tanga umepokea zaidi ya Sh156 bilioni kwa ajili ya kuboresha mazingira ya kujifunza na kufundishia.

Alisema uwekezaji huo ni sehemu ya juhudi za Serikali kuhakikisha wanafunzi wanapata mazingira bora ya elimu na kuongeza ubora wa huduma za elimu nchini.

Pia alimpongeza Profesa Mkenda na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa kuendelea kuunga mkono maonyesho hayo, akisema tukio hilo limeendelea kukua na kuboreshwa.

Kwa upande mwingine, Mkuu huyo wa Mkoa aliwataka wananchi wa Tanga na mikoa jirani kujitokeza kwa wingi katika Viwanja vya Usagara kushuhudia maonyesho hayo na kupata elimu kuhusu fursa mbalimbali zinazopatikana katika sekta ya elimu, ujuzi, sayansi na ubunifu.

Alisema maonyesho hayo pia yatawapa wananchi nafasi ya kujionea hatua ambazo Tanzania imepiga katika matumizi ya teknolojia, utafiti na ubunifu katika kutatua changamoto mbalimbali za jamii.

Uzinduzi rasmi wa maonyesho hayo unatarajiwa kufanyika Agosti 18, 2026, ukiongozwa na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda, huku Waziri Mkuu, Mwigulu Nchemba, akitarajiwa kuwa mgeni rasmi katika hafla ya kufunga maonyesho hayo Agosti 24.

Top News