Chuo cha Bahari Dar es Salaam (DMI) kimewahimiza vijana, hususan mabinti, kuchangamkia fursa za masomo katika sekta ya bahari, kikieleza kuwa wahitimu wa chuo hicho wana nafasi kubwa ya kupata ajira ndani na nje ya nchi kutokana na mahitaji makubwa ya wataalamu wa sekta hiyo.

Akizungumza na waandishi wa habari katika banda la DMI kwenye Maonesho ya Kilimo ya NaneNane Kitaifa yanayoendelea jijini Dodoma, Agosti 4, 2026,  Mkufunzi Msaidizi wa chuo hicho, Baharia Jackline Lema, amesema ushiriki wa DMI katika maonesho hayo unalenga kutoa elimu kwa umma kuhusu kozi mbalimbali zinazotolewa na chuo hicho pamoja na fursa zilizopo katika sekta ya bahari.

Lema ameeleza kuwa wanafunzi wanaochagua kusoma ubaharia hawatajutia uamuzi wao, kwani taaluma hiyo ina fursa nyingi za ajira na maendeleo ya kitaaluma.

Amesema DMI inatoa kozi mbalimbali ikiwemo unahodha, uhandisi ikiwemo mafuta na gesi pamoja na fani nyingine zinazohusiana na sekta ya bahari, amebainisha kuwa mwitikio wa wanafunzi umeendelea kuongezeka kila mwaka, ambapo zaidi ya wanafunzi 2,000 walihitimu katika mwaka wa masomo 2025/2026, jambo linaloonyesha kuongezeka kwa uelewa wa jamii kuhusu umuhimu wa sekta hiyo.

Aidha, amesema DMI ni chuo cha serikali kinachopokea wanafunzi wanaokidhi vigezo vya udahili na kwamba dirisha la maombi ya ngazi ya cheti na diploma litafunguliwa rasmi Agosti 23, 2026, huku udahili wa shahada na uzamili ukiendelea kwa mwaka wa masomo 2026/2027.

Lema amesema wahitimu wa DMI hupata nafasi za ajira katika taasisi mbalimbali za serikali ikiwemo TASHICO, TASAC na TPA, kampuni za usafirishaji, kampuni za mafuta na gesi,kampuni za usafirishaji na baadhi ya maeneo mengine ya kazi ndani na nje ya Tanzania kulingana na mahitaji ya soko la ajira duniani.

Akizungumzia dhana iliyokuwepo hapo awali kuwa ubaharia ni taaluma ya wanaume pekee, amesema idadi ya wanawake wanaojiunga na fani hiyo imeongezeka kwa kiwango kikubwa, hali ambayo imeondoa mtazamo huo na kuonyesha kuwa wanawake wana uwezo mkubwa wa kufanya vizuri katika sekta ya bahari.

Pia ameeleza namna wanafunzi wa DMI wanavyopata vipaumbele na fursa mbalimbali za ufadhili wa masomo pamoja na mikopo ya Serikali inayoratibiwa na HESLB, Samia Scholarship kwa baadhi ya programu, mikopo ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar pamoja na METFUND kwa wanaosoma kozi zinazohusiana na ubaharia.

Amesisitiza kuwa wahitimu wa DMI wameendelea kuwa miongoni mwa wataalamu wanaohitajika zaidi katika soko la ajira la kimataifa, jambo linaloifanya sekta ya bahari kuwa chaguo bora kwa vijana wanaotafuta taaluma yenye ajira za uhakika na mchango mkubwa katika maendeleo ya uchumi wa Taifa.







Farida Mangube Morogoro 

Katika kukabiliana na ujangili na usafirishaji holela wa nyara za Serikali, Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kimeanzisha utafiti wa kutumia panya buku wenye uwezo wa kunusa na kubaini nyara hizo katika maeneo mbalimbali ya usafirishaji.

Makamu Mkuu wa SUA, Profesa Raphael Chibunda, amesema utafiti huo ni sehemu ya jitihada za chuo hicho za kubuni teknolojia bunifu zitakazosaidia vyombo vya dola kudhibiti biashara haramu ya nyara za Serikali.

Profesa Chibunda alitoa kauli hiyo wakati Waziri Mkuu, Mwigulu Nchemba, alipotembelea banda la SUA katika Maonesho ya 88 ya Kanda ya Mashariki yanayoendelea mkoani Morogoro.

Alisema panya hao wamefundishwa kutumia uwezo wao wa kunusa kubaini nyara za Serikali na tayari wameanza kutumika kwa majaribio katika viwanja vya ndege na bandari.

Kwa upande wake, mtafiti kutoka Kituo cha Kudhibiti Wanyama Waharibifu wa Mazao (Pest Management Centre), Princus Mramba, alisema mradi huo ulianza miaka minne iliyopita na kwa sasa umefikia hatua nzuri ya utekelezaji.

Alisema baadhi ya panya hao wamepelekwa nchini Uturuki kushiriki katika shughuli za uokoaji kwa kusaidia kubaini watu waliofukiwa kwenye vifusi baada ya majanga.

Mbali na utafiti huo, Profesa Chibunda alisema SUA pia imeanzisha utafiti wa kutumia bundi kudhibiti panya waharibifu wa mazao mashambani.

Alieleza kuwa, kwa mujibu wa utafiti huo, bundi mmoja ana uwezo wa kula hadi panya 15 kwa siku, hivyo kuwa njia rafiki kwa mazingira katika kupunguza uharibifu wa mazao unaosababishwa na panya.

Aidha, alisema SUA inamiliki Hospitali ya Rufaa ya Wanyama inayotoa huduma za matibabu kwa wanyama wa kufugwa na wanyamapori. Aliongeza kuwa hospitali hiyo pia huwategua wanyama waliokwama kwenye mitego, kuwapatia matibabu na kuwarejesha katika mazingira yao.









 

Serikali kupitia Kampuni ya Mbolea Tanzania (TFC) imewahakikishia wakulima nchini upatikanaji wa mbolea ya kutosha kwa msimu wa kilimo wa mwaka huu, ikitangaza kuanza kwa usambazaji wa tani 33,000 za mbolea ya kupandia aina ya DAP zilizowasili nchini kupitia Bandari ya Dar es Salaam.

Akizungumza leo Agosti 4,2026 katika Maonesho ya 49 ya Kilimo ya Nanenane yanayoendelea kitaifa katika viwanja vya Dkt. John Samuel Malecela jijini Dodoma, Mkurugenzi wa Uendeshaji Biashara wa Kampuni ya Mbolea Tanzania (TFC), Lameck Borega, amesema kampuni hiyo imejipanga kuhakikisha wakulima wanapata mbolea kwa wakati, kwa bei nafuu na katika maeneo yote ya nchi.

Amesema TFC, ambayo ni kampuni inayomilikiwa kwa asilimia 100 na Serikali chini ya Wizara ya Kilimo, ina jukumu la kuhakikisha upatikanaji wa mbolea kwa wakulima wote ili kuongeza uzalishaji na kuimarisha usalama wa chakula nchini.

Bw.Borega amesema kwa msimu wa mwaka huu kampuni imepanga kusambaza takribani tani 200,000 za mbolea za aina mbalimbali, huku meli ya MV Aurora ikiwa tayari imewasili na tani 33,000 za mbolea ya DAP ambazo zimeanza kusafirishwa kwenda vituo vya TFC na kwa mawakala wake nchini kote.

"Mbolea hii imewasili kwa wakati muafaka wakati wakulima wengi wanaendelea kuandaa mashamba yao kwa ajili ya msimu mpya wa kilimo. Lengo letu ni kuhakikisha hakuna mkulima anayekosa mbolea kutokana na ucheleweshaji wa usambazaji," amesema Borega.

Aidha, amesema Serikali inaendelea kubeba sehemu kubwa ya gharama za mbolea kupitia mpango wa ruzuku ili kupunguza mzigo kwa wakulima. Alifafanua kuwa mfuko mmoja wa kilo 50 wa mbolea ya DAP ungegharimu karibu shilingi 200,000 bila ruzuku, lakini kutokana na msaada wa Serikali mkulima analipa karibu nusu ya gharama hiyo huku Serikali ikigharamia sehemu iliyobaki.

Amesema hatua hiyo ni sehemu ya dhamira ya Serikali ya kuongeza tija katika sekta ya kilimo kwa kuhakikisha pembejeo muhimu zinapatikana kwa gharama zinazomuduwa na wakulima.

Bw.Borega ameongeza kuwa baada ya kukamilika kwa usambazaji wa mbolea ya kupandia, Serikali inatarajia kuingiza nchini tani 40,000 za mbolea ya kukuzia aina ya Urea mwezi Septemba, hatua itakayowezesha wakulima kupata pembejeo zote muhimu katika kipindi sahihi cha uzalishaji.

"Niwaondoe wasiwasi wakulima wote nchini Serikali imejipanga kikamilifu kuhakikisha mbolea inapatikana kwa wakati na kwa mfumo wa ruzuku ili kila mkulima aweze kunufaika na kuongeza uzalishaji wa mazao," amesema 

Sambamba na hilo,Bw. Borega amewataka wakulima wanaotembelea Maonesho ya Nanenane kutembelea  banda la TFC ili kupata elimu ya matumizi sahihi ya mbolea, namna ya kunufaika na mfumo wa ruzuku na mahali pa kupata mbolea hizo.

Amesema TFC pia inaendelea kushiriki maonesho ya Nanenane katika kanda mbalimbali nchini ikiwemo Mbeya, Arusha, Mwanza, Simiyu, Iringa na Morogoro, ambako wakulima wanaendelea kupewa elimu ya kitaalamu kuhusu matumizi bora ya mbolea na njia rahisi za kuzipata kupitia mtandao wa vituo na mawakala wa kampuni hiyo.

Hata hivyo amesisitiza kuwa matumizi sahihi ya mbolea ni nguzo muhimu ya kuongeza tija ya kilimo, hivyo akawataka wakulima kutumia fursa ya maonesho hayo kupata elimu itakayowawezesha kuongeza uzalishaji na kuinua kipato chao.

Waswahili husema nyumba njema haikosi wageni na hii imedhihirika leo tarehe 4 Agosti, 2026 baada ya Spika wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar mhe Zubeir Ali Maulid kutembelea eneo la Hifadhi ya Ngorongoro.

Akiwa katika geti la Loduare Spika Maulid alipata taarifa ya vivutio vya eneo hilo iliiyotolewa na Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi Mariam Kobelo ambapo alielezwa kuendelea kuimarika kwa shughuli za uhifadhi,utalii na maendeleo ya jamii.

Aidha, haitoshi Spika Zubeir alielezwa kuhusiana na maajabu ya mchanga unaohama uliopo eneo la Olduvai ambapo mamia ya watu ambao mapenzi yao yamelega lega humiminika katika eneo hilo kuimarisha mapenzi.

Kwa mujibu wa simulizi za kihistoria kutokana na mchanga huo kuwa na asili ya sumaku wapendao wakifika mahali hapo penzi huwa motomoto na kuimarika.

Akizungumza baada ya ziara hiyo Spika Zubeir ametoa wito kwa watanzania kujenga utamaduni wa kutembelea vivutio vya utalii ili kujifunza na kupata utulivu.

Spika Zubeir ameipongeza Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro kwa kufanya kazi usiku na mchana katika kulinda uhifadhi, kusimamia utalii na maendeleo ya jamii.









 Waziri wa Kilimo wa Jamhuri ya Sudani Kusini, Mhe. Clement Juma Mbugoniwia, ametembelea banda la Taasisi ya Kuthibiti Ubora wa Mbegu Tanzania (TOSCI) katika Maonesho ya Kitaifa ya Nanenane yanayoendelea Nzuguni, mkoani Dodoma, kwa lengo la kujifunza mifumo inayotumika nchini katika kudhibiti na kuthibitisha ubora wa mbegu.

Waziri huyo akiwa ameambatana na mwenyeji wake, Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Bw. Gerald Mweli, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, alielezwa namna TOSCI inavyotekeleza jukumu lake la kuhakikisha mbegu zinazozalishwa na kusambazwa kwa wakulima zinakidhi viwango vya ubora vilivyowekwa.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mkurugenzi Mkuu wa TOSCI, Bw. Nyasebwa Chimagu, amesema taasisi hiyo iko tayari kushirikiana na Serikali ya Sudani Kusini katika kuimarisha mifumo ya udhibiti wa ubora wa mbegu, pamoja na kukuza uzalishaji na biashara ya mbegu bora za mazao ya kilimo.

Chimagu amesema miongoni mwa mifumo inayotumika na TOSCI ni mfumo wa kielektroniki wa uhakiki wa ubora wa mbegu kupitia lebo maalum za ubora. Mfumo huo unamwezesha mkulima kuhakiki uhalali na ubora wa mbegu alizonunua kwa kutumia simu ya kiganjani, kwa kuingiza namba maalum inayopatikana baada ya kukwangua lebo na kufuata maelekezo kupitia 14852#.

Amesema mkulima anaweza pia kupata huduma kwa kuwasiliana na TOSCI kupitia namba ya huduma kwa wateja isiyolipiwa 0800782424, hatua inayolenga kuongeza uelewa na uwezo wa wakulima katika kutambua mbegu zilizothibitishwa.

Katika ziara hiyo, viongozi hao pia walipata ufafanuzi kuhusu upatikanaji wa mbegu za awali, maarufu kama Early Generation Seed, ambazo ni muhimu katika mnyororo wa uzalishaji wa mbegu bora.

Kwa mujibu wa Chimagu, TOSCI inashirikiana na taasisi za utafiti, ikiwemo Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI), pamoja na sekta binafsi, katika kutambua na kuthibitisha aina mpya za mbegu kwa kuzingatia mahitaji ya soko na mazingira ya wakulima.

Aidha, amesema TOSCI inazingatia viwango vya kimataifa vya ISTA na OECD katika utekelezaji wa majukumu yake ya udhibiti na uthibitishaji wa ubora wa mbegu.

Amesema ushirikiano kati ya Tanzania na Sudani Kusini katika eneo hilo unaweza kusaidia kubadilishana uzoefu na maarifa kuhusu mifumo ya udhibiti wa ubora wa mbegu, pamoja na kuimarisha uzalishaji na biashara ya mbegu bora katika masoko ya ndani na kimataifa.







Na. Mwandishi Wetu – Dar es Salaam

Katibu Mkuu Ofisi ya Rais – Mipango na Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Mipango Dkt. Tausi Kida ameongoza kikao cha Makatibu Wakuu kwa niaba ya Mwenyekiti wa Kikao hicho ambaye ni Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) Dkt. Jim Yonazi kilicholenga kujadili utendaji wa Mradi wa Mabasi Yaendayo Haraka -BRT leo 04 Agosti, 2026 kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi ya Waziri Mkuu Jijini Dar es Salaam.

Dkt. Tausi ameongoza kikao hicho kilichoratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu kwa lengo la kupokea na kujadili taarifa ya timu ya wataalam kuhusu utendaji wa Mradi huo ambapo imeelezwa kuwa lengo la Mradi huo ni kutatua changamoto ya msongamano wa magari katika Mkoa wa Dar es salaam kwa kuboresha huduma ya usafiri kwa Jamii.

Kikao hicho kilijumuisha wataalam kutoka Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, Tume ya Taifa ya Mipango, Ofisi ya Waziri Mkuu - TAMISEMI, Wizara ya Fedha, Wizara ya Ujenzi, WIzara ya Uchukuzi, Msajili wa Hazina, Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini (LATRA), Wakala wa Mabasi Yaendayo Haraka (DART), Kampuni ya Mabasi Yaendayo Haraka Dar es Salaam (UDART) na Kituo cha Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP Centre), Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), Kituo cha Taifa cha Kuhifadhi Data Kimtandao (NIDC). 

Aidha, Dkt. Tausi ametumia kikao hicho kuwakumbusha watendaji kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa weledi huku akieleza lengo la Serikali la kuendelea kuwapatia wakazi wa jiji la Dar es salaam usafiri bora, wa haraka na salama na kuendelea kupunguza msongamano wa magari ili kuokoa muda wa safari na kuboresha usalama barabarani.

“Mradi huu utumike kama ilivyokusudiwa na kuendelea kujiratibu vyema ili kuendelea kutoa huduma bora za usafiri kwa wananchi,” alisema Dkt. Tausi














Na Mwandishi Wetu, DSM.

Serikali kupitia Mamlaka ya hifadhi ya eneo la Ngorongoro (NCAA) kwa kushirikiana na Bodi ya Mikopo ya wanafunzi wa elimu ya huu (HESLB) imeanzisha mfuko wa Ngorongoro Scholarship Fund kwa lengo la kuwezesha wanafunzi wanaoishi ndani ya hifadhi ya Ngorongoro kupata fursa ya masomo ya elimu ya juu kupitia ufadhili Ngorongoro Fund.

Akizungumza wakati wa mkutano wa waandishi wa Habari Jijini Dar es salaam kwa niaba ya kamishna wa Uhifadhi, Kamishna msaidizi mwandamizi wa uhifadhi anayesimamia idara ya Maendeleo ya Jamii Gloria Bideberi ameeleza kuwa Program hiyo inalenga kuboresha maisha ya jamii zinazoishi ndani ya hifadhi, ambapo kwa kushirikiana na bodi ya mikopo ya elimu ya juu watahakikisha kila mtoto anayeishi ndani ya hifadhi hiyo anayekidhi vigezo anapata nafasi ya kupata ufadhili wa elimu ya juu.

“Kupitia Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu ufadhili huu utasaidia kuondoa malalamiko ya upendeleo, taratibu zote za ufadhili wa vijana wetu zitakuwa wazi kwa kuzingatia vigezo vilivyowekwa tukitambua kuwa elimu ndiyo msingi wa kuwawezesha wananchi kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya kiuchumi, kijamii na mazingira” amesema kamishna Bideberi.

Ameongeza kuwa Ngorongoro Fund inaongozwa na kauli mbiu isemayo "Elimu Endelevu kwa Maendeleo ya Jamii na Uhifadhi" itakwenda kufadhili watoto wa kitanzania waliodahiliwa katika vyuo vilivyopo ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kunufaisha vijana watakaojikita katika masomo ya uhifadhi wa Wanyamapori na misitu, Malikale na utalii na hapo baadaye wigo utaendelea kutanuliwa.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa HESLB Dkt. Bill Kiwia amesema kuanzia mwaka wa masomo 2026/2027, Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB), kwa kushirikiana Ngorongoro, itaanza kutoa ufadhili huo maalum kwa wanafunzi kutoka eneo la Hifadhi ya Ngorongoro watakaosoma fani zinazohusiana na uhifadhi wa maliasili, usimamizi wa wanyamapori, pamoja na taaluma nyingine zitakazoainishwa katika Mwongozo wa Utoaji wa Scholarship hiyo.

Dkt. Kiwia ameeleza kuwa hatua ya kwanza ya utekelezaji wa mpango huu utaanza kwa kutoa ufadhili kwa wanafunzi 15, ambapo Ngorongoro imetenga shilingi milioni 99 kugharamia masomo ya ufadhili na kuwawezesha vijana hao kupata elimu ya juu, kujenga wataalamu watakaosaidia kuhifadhi rasilimali za Taifa, na kuchochea maendeleo endelevu ya jamii zinazozungukaHifadhi ya Ngorongoro.

Kwa ushirikiano wa karibu kati ya HESLB na NCAA, tayari tumekamilisha Mwongozo Maalum wa Utoaji wa Scholarship ya NCAA ambapo mwongozo huo umeweka vigezo, taratibu na masharti ya utoaji wa ufadhili huo kwa wanafunzi wanaotoka katika jamii zinazoishi ndani ya Hifadhi ya Ngorongoro kwa kutambua programu mahususi zitakazopewa kipaumbele, hususan zile zinazohusiana na uhifadhi wa maliasili, usimamizi wa wanyamapori na taaluma nyingine zinazochangia maendeleo endelevu ya eneo la Ngorongoro na Taifa kwa ujumla.

Sambamba na mwongozo huo, HESLB imekamilisha maandalizi ya mfumo wa kidijitali wa kupokea na kuchakata maombi ya scholarship ambapo hii dirisha la kupokea maombi litafunguliwa tarehe 15 Agosti, 2026, kwa sasa Ngorongoro na bodi ya mikopo zinaendelea kutoa elimu na uhamasishaji kwa waombaji watarajiwa ili kuwawezesha kuelewa vigezo vya scholarship hii na kujaza maombi yao kwa usahihi na kwa wakati.

Kabla makubaliano haya ya leo, Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro ilikuwa ikitekeleza ufadhili huu kupitia Baraza la Wafugaji ambapo mpaka mwaka wa fedha uliopita 2025/2026 zaidi ya watu elfu kumi na tano kutoka ndani ya hifadhi wamepatiwa ufadhili katika nyanja mbalimbali ikiwemo ualimu, udaktari, uhandisi, uhasibu, wataalamu wa uhifadhi na kada nyingine nyingi zinazochangia maendeleo ya jamii na taifa kwa ujumla.












Na Victor Masangu, Kibaha

Katika kupambana na wimbi la umasikini na kuachana na kuwa tegemezi kwa wanawake Mwenyekiti wa Jumuiya ya wanawake (UWT) Wilaya ya Kibaha mjini Elina Mgonja ameamua kutoa darasa maalumu kwa ajili ya kufundisha mafunzo ya ujasiriamali na jinsi ya kutenghheneza bidhaa kwa wanawake mbali mbali kwa lengo la kuweza kuwasaidia kuachana na kuwa tegemezi ikiwa sambamba na kujikwamua kiuchumi

Hayo yamebaishwa wakati wa ziara yake maalumu yenye lengo la kuweza kukutana na baadhi ya makundi ya wanawake kwa ajili ya kutoa darasa la mafunzo mbali mbali ya ujasiliamali yenye lengo la kuwaongozea ujuzi na elimu ambayo itawasaidia katika kutengeneza biadha za aina tofauti.

Mwenyekiti huyo ametoa darasa la mafunzo hayo kwa wanawake wa jumuiya ya UWT katika kata mbili za Msangani na Kata ya Mkuza ambapo zaidi ya wanawake 100 wameweza kupatiwa mafunzo mbali mbali ya kutengeneza bidhaa mbali mbali ikiwemo kufundisha jinsi ya kutengeneza bidhaa za batiki, sabuni za kuogea, sabuni za chooni,shampuu kwa ajili ya nywele.

Mgonja amebainisha kwamba ametoa kutoa elimu hiyo ya darasa la mafunzo ya ujasiriamali bure bila malipo ikiwa ni utekelezaji wake wa ahadi ambayo aliitoa wakati akiwa katika ziara yake ya kuwashukuru wanawake hao ambao waliweza kukiheshimisha chama wakati wa uchaguzi mkuu wa mwaka 2025 ambapo waliweza kupiga kura za kisdindo.

"Ahadi ni deni kwa hiyo mimi kama Mwenyekiti wa UWT nimekuja kuwapa elimu na mafunzo mbali mbali ya ujasiliamali bila malipo ya iana yoyote na kwamba mafunzo hayo ni moja ya ahadi yangu ambayo niliitoa wakati nikiwa katika ziara yangu ya kutoa shukrani kwa wanawake kukipigia chama cha mapinduzi kura nyingi za kishindo katika uchaguzi mkuu,"amebainisha Mwenyekiti Mgonja.

Kwa upande wake Katibu katibu wa UWT Cesilia Ndaru amewahimiza wanawake kuhakikisha kwamba wanatumia fursa mbali mbali za ujasiriamali na kuachana kabisa na tabia ya kuwa na majungu na kuzungumza maneno ambayo hayana faida yoyote na badala yake wajiunge katika vikundi vya ujasiriamali.

Naye mjumbe wa kamati ya utekeelzaji wa UWT Zainabu Gama amebainisha kwamba darasa la mafunzo hayo yataweza kuwasaidia kwa kiasi kikubwa wanawake hao katika kujiongezea kipato na kujikwamu kiuchumi.

Nao baadhi ya wanawake kutoka kata za Msangani na Mkuza ambao wameweza kupata fursa ya kupata elimu hiyo ya kutengeneza bidhaa mbali mbali wamesema wamempongeza Mwenyekiti wa UWT kwa kuwapatia darasa hilo la elimu ambayo itakwenda kuwasaidia kwa kiasi kikubwa katika kujikwamua na wimbi la umasikini na kujikwamua kiuchumi.

Ziara maalumu ya Mwenyekiti wa UWT Kibaha mjini ambayo imendaliwa mahususi kwa ajili ya kutekeleza ahadi yake ambayo aliitoa ya kuwa na darasa la kutoa elimu ya ujasiriamali na jinsi ya kutengeneza bidha bila malipo ambapo ameanza mafunzo hayo katika kata mbili za Msangani pamoja na Mkuza.








Top News