Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, leo ameongoza zaidi ya washiriki 13,000 katika mbio za NBC Dodoma Marathon 2026 zilizofanyika katika Uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma, huku akiipongeza Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) kwa kufanikisha ukusanyaji wa shilingi bilioni 1 zitakazotumika kuokoa maisha ya maelfu ya Watanzania kupitia miradi ya afya ya mama na mtoto.

Fedha hizo zitasaidia utekelezaji wa maeneo matatu muhimu ya kijamii ambayo ni kupunguza vifo vya akina mama na watoto wakati wa kujifungua, kugharamia upasuaji wa watoto wenye matatizo ya moyo, pamoja na kuimarisha huduma za upandikizaji wa uloto kwa watoto wanaoishi na ugonjwa wa selimundu (Sickle Cell).

Mbio hizo, ambazo zimeendelea kujijengea hadhi kama moja ya matukio makubwa zaidi ya michezo nchini, zilihusisha washiriki kutoka Tanzania na mataifa mbalimbali, huku zikishuhudia ushindani mkubwa kati ya wanariadha wa Tanzania na Kenya katika mbio za kilomita 21 na 42. Dkt. Nchemba, pamoja na viongozi mbalimbali wa Serikali, taasisi na sekta binafsi, walishiriki mbio za kilomita tano (5) kuhamasisha mazoezi na maisha yenye afya.

Akizungumza wakati wa hafla ya kukabidhi zawadi kwa washindi na wadau wa mbio hizo, Dkt. Nchemba alisema mafanikio ya NBC Dodoma Marathon yanaonesha jinsi ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi unavyoweza kuleta matokeo yenye manufaa makubwa kwa jamii.

Alisema ongezeko la washiriki kutoka 1,500 mwaka 2020 hadi zaidi ya 13,000 mwaka 2026 ni ushahidi wa mwamko mkubwa wa Watanzania katika kushiriki michezo, kuzingatia afya zao na kuunga mkono shughuli za maendeleo kupitia michezo.

"NBC Dodoma Marathon imekuwa zaidi ya mashindano ya riadha. Leo ni jukwaa linalounganisha Watanzania na marafiki kutoka mataifa mbalimbali kwa lengo la kufanya jambo kubwa zaidi—kuokoa maisha. Nawahimiza Watanzania kujenga utamaduni wa kufanya mazoezi mara kwa mara ili kujikinga dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza kama vile kisukari, shinikizo la damu, magonjwa ya moyo na figo," alisema Dkt. Nchemba.

Aidha alisema Serikali itaendelea kuboresha miundombinu ya barabara katika Jiji la Dodoma kwa kupanua na kuboresha barabara muhimu, hatua itakayorahisisha shughuli za usafirishaji na wakati huo huo kuongeza usalama wa washiriki wa mbio hizo katika miaka ijayo.

Waziri Mkuu pia aliutaka uongozi wa Mkoa wa Dodoma kuendelea kuziunga mkono mbio hizo kutokana na mchango wake mkubwa katika kukuza uchumi wa jiji hilo kupitia ongezeko la wageni, shughuli za utalii wa ndani, biashara za hoteli, migahawa, usafiri na huduma nyingine zinazochochewa na tukio hilo.

Awali, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Bi. Rosemary Senyamule, alisema NBC Dodoma Marathon imeendelea kuwa kichocheo muhimu cha uchumi wa mkoa huo kwa kuongeza mzunguko wa fedha na kutoa fursa kwa wafanyabiashara wadogo na wakubwa kila mwaka.

Aliishukuru Benki ya NBC kwa kuendelea kuwa mshirika mkubwa wa maendeleo ya Mkoa wa Dodoma kupitia uwekezaji wake katika afya, michezo na maendeleo ya jamii.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NBC, Bw. Theobald Sabi, alisema mafanikio ya mbio hizo yanaakisi dhamira ya benki hiyo ya kuendelea kutumia biashara kama chachu ya kuleta maendeleo ya kijamii.

Alisema kati ya fedha zilizokusanywa, shilingi milioni 600 zimeelekezwa moja kwa moja katika utekelezaji wa malengo makuu ya NBC Dodoma Marathon kupitia taasisi tatu zinazotoa huduma muhimu za afya nchini.

Katika hafla hiyo, Dkt. Nchemba na Bw. Sabi walikabidhi hundi za misaada ambapo: Shilingi milioni 200 zilikabidhiwa Taasisi ya Benjamin Mkapa kwa ajili ya kupanua programu ya ufadhili wa wakunga ili kuboresha huduma za afya ya uzazi, Shilingi milioni 200 zilikabidhiwa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) kwa ajili ya kugharamia upasuaji wa watoto wenye matatizo ya moyo na Shilingi milioni 200 zilikabidhiwa Hospitali ya Benjamin Mkapa kusaidia huduma za upandikizaji wa uloto kwa watoto wenye ugonjwa wa selimundu.

"Mafanikio haya yanatokana na dhamira yetu ya kuhakikisha mafanikio ya biashara yanaenda sambamba na ustawi wa jamii. Tunawashukuru washiriki wote, wadhamini na wadau mbalimbali waliochangia kufanikisha NBC Dodoma Marathon 2026. Ushirikiano huu umewezesha kuokoa maisha ya Watanzania wengi," alisema Bw. Sabi.

Alitoa shukrani maalumu kwa wadhamini wakuu wa mbio hizo akiwemo Sanlam Allianz, GSM Group, Vodacom Tanzania, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) pamoja na wadau wengine waliochangia mafanikio ya tukio hilo.

Katika mbio za kilomita 42 (Full Marathon) kwa upande wa wanaume, mwanariadha kutoka Kenya Edwin Koech aliibuka mshindi wa kwanza kwa kutumia muda wa saa 2:05:12, akifuatiwa na Vitalis Kibiwott aliyemaliza kwa saa 2:12:18.

Kwa upande wa wanawake, Agnes Ngolo wa Kenya alitwaa ushindi kwa kutumia muda wa saa 2:32:36, huku Jacinta Chepkoech, pia kutoka Kenya, akimaliza wa pili kwa muda wa saa 2:33:26.

Washindi wa nafasi ya kwanza hadi ya kumi walizawadiwa fedha taslimu, ambapo washindi wa kwanza wa mbio za kilomita 42 kwa wanaume na wanawake kila mmoja alijishindia Tsh milioni 11.5.

Katika mbio za kilomita 21 (Half Marathon) kwa wanaume, Bernard Geay wa Tanzania aliibuka mshindi wa kwanza kwa muda wa saa 1:02:46, akifuatiwa na Simon Kelenzoke wa Kenya (1:02:57), huku nafasi ya tatu ikichukuliwa na Michael Geay wa Tanzania kwa muda wa 1:02:59.

Kwa upande wa wanawake, Magdalena Shauri wa Tanzania aliibuka mshindi wa kwanza kwa muda wa 1:08:59, akifuatiwa na Doreen Chetzop wa Kenya aliyemaliza kwa muda wa 1:10:36.

Washindi wa kwanza wa mbio za kilomita 21 kwa wanaume na wanawake walijishindia Tsh milioni 5.5, huku washindi wa pili wakiondoka na Tsh milioni 2.5.

NBC Dodoma Marathon imeendelea kuthibitisha kuwa si tu tamasha kubwa la michezo nchini, bali pia ni jukwaa la kuhamasisha afya, kuunganisha jamii, kukuza uchumi wa Jiji la Dodoma na kuchangia moja kwa moja kuboresha huduma muhimu za afya kwa Watanzania.


Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, (katikati) akimkabidhi mfano wa hundi yenye thamani ya Tsh milioni 200 kwa muwakilishi wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) (wanne kushoto) iliyotolewa na Benki ya NBC kwa ajili ya kugharamia upasuaji wa watoto wenye matatizo ya moyo kupitia mbio za NBC Dodoma Marathon zilizofanyika leo kwenye Uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma. Wanaoshuhudia ni pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Bi. Rosemary Senyamule (wa tatu kushoto), Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NBC Bw Theobald Sabi (wa nne kulia), Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya benki ya NBC , Dkt. Elirehema Doriye (wa pili kushoto), Mkurugenzi Mtendaji wa SanlamAllianz, wadhamini wakuu wa mbio hizo, Bw Julius Magabe (kushoto) na viongozi wengine kutoka serikalini na wadau wa mbio hizo.




Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, (katikati) akimkabidhi mfano wa hundi yenye thamani ya Tsh milioni 200 kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Benjamin Mkapa, Profesa Abel Makubi (wa tatu kushoto) iliyotolewa na Benki ya NBC kwa ajili ya kusaidia huduma za upandikizaji wa uloto kwa watoto wenye ugonjwa wa selimundu (sicke cell)kupitia mbio za NBC Dodoma Marathon zilizofanyika leo kwenye Uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma. Wanaoshuhudia ni pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Bi. Rosemary Senyamule (wa pili kushoto), Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NBC Bw Theobald Sabi (wa pili kulia), Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya benki hiyo, Dkt. Elirehema Doriye (kushoto) na viongozi wengine kutoka serikalini na wadau wa mbio hizo.


Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, (katikati) akimkabidhi mfano wa hundi yenye thamani ya Tsh milioni 200 kwa muwakilishi wa Taasisi ya Benjamin Mkapa Foundation (wanne kushoto) iliyotolewa na Benki ya NBC kwa ajili ya kwa ajili ya kupanua programu ya ufadhili wa wakunga ili kuboresha huduma za afya ya uzazi kupitia mbio za NBC Dodoma Marathon zilizofanyika leo kwenye Uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma. Wanaoshuhudia ni pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Bi. Rosemary Senyamule (wa tatu kushoto), Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NBC Bw Theobald Sabi (wa nne kulia), Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya benki ya NBC , Dkt. Elirehema Doriye (wa pili kushoto), Mkurugenzi Mtendaji wa SanlamAllianz, wadhamini wakuu wa mbio hizo, Bw Julius Magabe (kushoto) na viongozi wengine kutoka serikalini na wadau wa mbio hizo.


Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, (wa tatu kushoto) akikabidhi mfano wa hundi yenye thamani ya sh mil 5.5 kwa mwanariadha kutoka Tanzania, Magdalena Shauri alieibuka mshindi wa kwanza (kwa upande wa wanawake) wa mbio za km 21 za NBC Dodoma Marathon, zilizofanyika leo kwenye Uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma. Wanaoshuhudia ni pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NBC Bw Theobald Sabi (wa pili kulia) na viongozi wengine kutoka serikalini na wadau wa mbio hizo.



Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, (kushoto) akikabidhi mfano wa hundi yenye thamani ya sh mil 11.5 kwa mwanariadha kutoka Kenya, Edwin Koech alieibuka mshindi wa kwanza (kwa upande wa wanaume) wa mbio za km 42 za NBC Dodoma Marathon, zilizofanyika leo kwenye Uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma. Wanaoshuhudia ni pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NBC Bw Theobald Sabi (kulia)

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi ametembelea na kukagua maendeleo ya ujenzi wa Uwanja wa Arusha, utakaotumika katika michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika mwaka 2027 (AFCON 2027), unaojengwa Jijini Arusha.

 Makamu wa Rais amepongeza maendeleo ya ujenzi wa uwanja huo, ambapo amesema ni faraja kuona ahadi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan aliyoitoa ili kuvutia michuano hiyo kufanyika nchini Tanzania, inatakelezwa kikamilifu. Amemshukuru Mhe. Rais kwa kuendelea kutoa fedha ili kuhakikisha uwanja huo unakamilika kwa wakati.

Aidha, Makamu wa Rais ameishukuru Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo pamoja na mkoa wa Arusha, Wakandarasi na Mshauri Elekezi kwa kazi kubwa waliyofanya katika Uwanja huo.

 Makamu wa Rais amewataka Viongozi wa Wizara pamoja na Mkoa wa Arusha kusimamia vema agizo la Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan la kuhakikisha barabara zinazotumika katika kufika uwanjani hapo zinakamilika kwa wakati.

Awali Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mhe. Amos Makala, amemueleza Makamu wa Rais, maendeleo ya ujenzi wa uwanja huo ambao umefikia asilimia 88, ukitarajiwa kukamilika ifikapo mwishoni mwa mwezi Agosti, 2026.

 Uwanja wa Arusha, utakapokamilika, mbali na michezo, unatarajiwa kuwa kivutio cha utalii ukiwa umebeba alama ya Mlima Kilimanjaro, Madini ya Tanzanite na Bendera ya Taifa.












 



SAME.

MKUU wa Wilaya ya Same, Kasilda Mgeni, amewaonya wananchi wanaojihusisha na uchimbaji haramu wa madini ndani ya mita 60 kutoka kwenye vyanzo vya maji, akisisitiza kuwa hakuna mtu au mwekezaji mwenye kibali cha kufanya shughuli za uchimbaji huo.

Amesema Serikali ya wilaya imeanza kuwachukulia hatua za kisheria, kwa lengo la kulinda vyanzo vya maji, mazingira na maslahi ya wananchi.

Hatua hiyo imekuja jana baada ya Kasilda, akiambatana na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya wilaya pamoja na wataalamu kutoka Ofisi ya Madini na Bonde la Mto Pangani, kutembelea baadhi ya maeneo yanayofanyika uchimbaji haramu wa madini na kujionea uharibifu mkubwa wa mazingira katika vyanzo vya maji vilivyopo Kata ya Mhezi.

Kasilda alisema ni kosa kisheria kuanza shughuli za uchimbaji wa madini bila kuwa na leseni au kibali kutoka Ofisi ya Madini, pamoja na kufanya shughuli yoyote ndani ya umbali wa mita 60 kutoka kwenye vyanzo vya maji bila kibali kutoka Bonde la Mto Pangani.

Alibainisha kuwa serikali imeanza kuwachukulia hatua wahusika wote ili kunusuru uharibifu wa mazingira na athari zinazoweza kujitokeza kutokana na shughuli hizo haramu.

"Ni kosa kisheria kuanza kuchimba madini bila kuwa na leseni au kibali husika kutoka Ofisi ya Madini na kufanya shughuli yoyote ndani ya mita 60 kutoka kwenye chanzo cha maji bila kibali kutoka Ofisi za Bonde. Wote wanaohusika tumeanza kuwashughulikia mara moja kwa lengo la kunusuru uharibifu na athari kubwa zinazoweza kutokea kutokana na uchimbaji huo haramu," alisema Kasilda.








NA DENIS MLOWE, IRINGA


MBUNGE wa Jimbo la Iringa Mjini, Fadhili Ngajilo, ametoa wito kwa wananchi, wadau wa michezo, wafanyabiashara na wazawa wa Iringa waliopo ndani na nje ya mkoa kushirikiana kuanzisha mfuko maalumu utakaowezesha kurejeshwa kwa timu ya Ligi Kuu Tanzania Bara itakayoiwakilisha Iringa.

Ngajilo alitoa kauli hiyo wakati wa kukabidhi vifaa vya michezo kwa timu 16 zilizofuzu hatua ya 16 bora ya mashindano ya Ngajilo Super League 2026 yaliyofanyika katika Uwanja wa Samora mjini Iringa.

Alisema baada ya miaka 15 tangu kuanzishwa kwa mashindano hayo mwaka 2010, sasa umefika wakati wa kuyatumia kama msingi wa kuimarisha maendeleo ya soka na kufanikisha ndoto ya mkoa kuwa na timu ya Ligi Kuu.

"Majadiliano ya kuwa na timu ya Ligi Kuu yamekuwa mengi sasa umefika wakati wa kugeuza maneno kuwa vitendo kwani Iringa inahitaji timu itakayobeba heshima na kuitangaza mkoa wetu nchini," alisema Ngajilo.

Alisisitiza kuwa timu hiyo haitakuwa mali ya wilaya au jimbo moja bali ya Mkoa mzima wa Iringa, akiwataka wananchi wa Kilolo, Mufindi, Isimani, Kalenga, Iringa Mjini pamoja na wazawa wanaoishi Dar es Salaam, Dodoma, Mbeya, Njombe, Morogoro na maeneo mengine kushiriki katika ujenzi wa timu hiyo.

Ngajilo alisema changamoto kubwa si kununua timu bali ni kuimudu kifedha, hivyo akashauri kuanzishwa mfumo wa kisasa wa usajili wa wanachama na uchangiaji wa fedha kwa njia za kidijitali ili kuhakikisha timu inakuwa na chanzo cha mapato cha uhakika.

Alieleza kuwa hata michango midogo ya shilingi 1,000 kwa mwezi kutoka kwa maelfu ya wananchi inaweza kuwa msingi wa kuiendesha timu kwa ufanisi, huku akipendekeza kuundwa kwa kamati maalumu ya fedha itakayosimamia ukusanyaji na matumizi ya michango hiyo.

Ngajilo aliwataka viongozi wa soka kuanza kujenga mifumo imara ya kifedha kabla ya kuanza mchakato wa kununua timu, akisema ni muhimu kuhakikisha kuna fedha za kutosha kwa ajili ya mishahara ya wachezaji, safari, malazi, vifaa na mahitaji mengine ya uendeshaji.

Aidha aliwahimiza wadau wengine kujitokeza kuunga mkono Ngajilo Super League ili maendeleo ya soka yasitegemee mfadhili mmoja pekee, huku akiwapongeza viongozi wa Chama cha Soka Wilaya ya Iringa (IDFA) kwa usimamizi mzuri wa mashindano hayo.

Katibu wa IDFA, Yahaya Mpelembwa, alimpongeza Mbunge Ngajilo kwa kuendelea kuwekeza katika maendeleo ya soka kwa miaka mingi na kusema mchango wake umeiwezesha ligi hiyo kukua kutoka ngazi ya Manispaa hadi kushirikisha timu kutoka majimbo ya Iringa Mjini, Isimani na Kalenga.

Alisema timu 16 zilizofuzu zimepatikana baada ya ushindani mkali wa ligi na sasa zitacheza hatua ya mtoano (knockout) hadi kupatikana bingwa atakayewakilisha Wilaya ya Iringa katika mashindano ya ngazi ya mkoa.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa IDFA, Joel Musiba, alisema Ngajilo ameendelea kuwa mdhamini mkuu wa ligi hiyo kwa misimu zaidi ya mitano bila ubaguzi, jambo lililochochea ukuaji wa soka la wilaya.

Musiba alisema chama hicho hakifanyi siasa bali kina wajibu wa kushirikiana na wadau wote wanaosaidia maendeleo ya michezo, akiwataka viongozi wa timu kuhakikisha wanathamini wadhamini kwa kuvaa jezi zenye nembo ya mdhamini rasmi wa mashindano.

Pia alimuomba Mbunge huyo kuendelea kuisaidia timu itakayotwaa ubingwa wa Ngajilo Super League katika safari yake ya kushiriki mashindano ya ngazi ya mkoa ili kuongeza nafasi ya Iringa kupata timu itakayopanda madaraja hadi kufikia Ligi Kuu Tanzania Bara.

Mashindano ya Ngajilo Super League yameendelea kuwa jukwaa muhimu la kuibua vipaji vya soka na kuimarisha ushindani wa timu za wilaya, huku wadau wakiamini kuwa yanaweza kuwa nguzo ya kurejesha hadhi ya soka la Mkoa wa Iringa.





Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), kwa kushirikiana na Chuo Kikuu cha Cambridge cha Uingereza, wameaanzisha utafiti wa vinasaba unaolenga kuboresha matibabu ya saratani ya tezi kwa watoto nchini Tanzania na ukanda wa Afrika.

Akieleza kuhusu utafiti huo, Dkt. Advera Ngaiza, Bingwa wa Uchunguzi wa Magonjwa ya Saratani amesema mradi huo utahusisha uchukuaji wa sampuli za vinasaba na tishu kutoka kwa watoto wenye saratani ya tezi nchini Tanzania. 

Amesema sampuli hizo zitachakatwa katika Maabara Kuu ya MNH, huku uchunguzi wa kina wa kisayansi ukifanyika ili kuelewa kwa nini matibabu ya sasa hayatoi matokeo mazuri kwa watoto wa Kiafrika. 

"Lengo letu ni kugundua dawa salama, sahihi na yenye ufanisi mkubwa zaidi itakayosaidia kutibu saratani ya tezi kwa watoto katika ukanda wa Afrika."

Hatua hii inakuja baada ya kubainika kuwa mifumo mingi ya sasa ya matibabu haitoi matokeo yanayotarajiwa kwa watoto wa ukanda huu wa afrika ikilinganishwa na maeneo mengine duniani. 

Kupitia utafiti huu, watafiti wanatarajia kuweka msingi wa maendeleo ya tiba zinazozingatia tofauti za vinasaba, hatua ambayo inaweza kuleta mapinduzi makubwa katika huduma za matibabu ya saratani kwa watoto barani Afrika.






 


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo Julai 25, 2026 ameongoza Maadhimisho ya Siku ya Kumbukumbu ya Mashujaa yaliyofanyika katika Uwanja wa Mashujaa, Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma.

Rais Samia aliwasili katika viwanja vya maadhimisho na kupokelewa kwa heshima rasmi za kijeshi, kabla ya kupokea heshima ya wimbo wa Taifa la Tanzania na wimbo wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Katika kilele cha maadhimisho hayo, Rais Samia aliweka mkuki na ngao kwenye Mnara wa Mashujaa ikiwa ni ishara ya kutoa heshima kwa mashujaa waliojitolea kwa ujasiri na uzalendo kwa ajili ya Taifa.

Maadhimisho hayo yalihudhuriwa na viongozi wa Serikali, vyombo vya ulinzi na usalama, wanajeshi wastaafu, viongozi wa dini pamoja na wananchi na wageni mbalimbali.

Siku ya Kumbukumbu ya Mashujaa huadhimishwa tarehe 25 Julai ya kila mwaka kwa lengo la kuwakumbuka na kuwaheshimu mashujaa waliopigania uhuru wa nchi na wale waliojitolea kulinda amani, usalama na maslahi ya Taifa.
Na Seif Mangwangi, Michuzi TV, Arusha

SERIKALI imeipongeza Menejimenti na uongozi wa chuo cha ufundi Arusha (ATC), kutokana na bunifu mbalimbali zinazoendelea kufanywa chuoni hapo ikiwemo ujenzi wa karakana ya kisasa kwaajili ya kufundishia na uzalishaji wa bidhaa mbalimbali.

Pongezi hizo zimetolewa na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Hussein Mohamed Omar, 24Julai 2026 jijini Arusha katika ziara yake ya kikazi chuoni hapo.

Dkt.Omar amesema ujenzi wa karakana hiyo ya kufundishia (Teaching Industry), utasaidia ongezeko kubwa la udahili wa wanafunzi chuoni hapo pamoja na kutoa fursa ya ajira kwa wanafunzi watakaopata elimu chuoni hapo.

Amesema Menejimenti ya chuo hicho chini ya Mkuu wake wa chuo Profesa Mussa Chacha pamoja na uongozi wa bodi ya chuo unastahili kupongezwa kwa kuwa umekuwa ukitafsiri sera ya Elimu kwa vitendo.

" Kwa niaba ya Serikali napenda kuwapongeza sana kuwekeza katika Ubunifu, lakini pia kwa kutafsiri sera ya Elimu kwa vitendo, ujenzi wa Karakana hii ni ubunifu wa hali ya juu, utaongeza udahili wa wanafunzi lakini pia kutoa ajira kwa wanafunzi watakaopata Elimu ya ufundi hapa hapa chuoni," amesema na kuongeza:

"Na wanafunzi wengine watakaofaulu vizuri pia wataajiriwa hapa hapa katika Karakana hii kwaajili ya kuzalisha bidhaa mbalimbali ambazo zitatumika ndani na nje ya nchi," amesema.

Dkt. Omar amesema kuwa tafsiri ya Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan ni kutafsiri Sera ya Elimu na maono ya dira ya Taifa ya 2050 ya kuhakikisha watanzania wengi wanapata elimu na Ujuzi wa kujiajiri wenyewe.

"Chuo cha Ufundi Arusha (ATC) kinaendelea kuimarisha elimu ya ufundi nchini kupitia ujenzi wa Kiwanda cha Uzalishaji (Industrial Workshop), mradi unaolenga kuwapa wanafunzi ujuzi wa vitendo, uzoefu wa kazi na kuwaandaa kwa soko la ajira," amesema Dkt Omar.

Kupitia kiwanda hicho, wanafunzi watashiriki katika uzalishaji wa bidhaa mbalimbali ikiwemo kuchonga vipuri vya magari, kupata uzoefu wa kazi, kuongeza uwezo wa kujiajiri au kuajiriwa, na hivyo kujipatia kipato wakati wa masomo.

Mkuu wa Chuo cha Ufundi Arusha, Prof. Musa Chacha, amesema mradi huo unaunga mkono Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kwa kuzalisha wahitimu wenye ujuzi unaokidhi mahitaji ya uchumi wa kisasa.

Amesema chuo chake kimeshaanza uzalishaji wa mita janja zinazotumika kusoma Dira ya maji kwa malipo ya kabla (pre paid bill), hatua inayoonyesha dhamira ya chuo kuunganisha elimu, teknolojia na maendeleo ya viwanda nchini.

Prof. Chacha amesema kiwanda hicho kitatumika pia kufanya uzalishaji wa mita hizo janja ambazo zitasambazwa kwa mamlaka za maji nchini ambazo zitakuwa tayari kuanza kuzitumia.

Meneja msimamizi wa MRADI wa Ujenzi wa kiwanda Cha Kufundishia (Teaching Industry) Mhandisi, Elineema Willium amesema mradi huo umewezeshwa na Serikali ya Tanzania kwa kushirikiana na Serikali ya Austria kupitia mkopo wa masharti nafuu.

Mhandisi Msuya amesema kuwa mradi huo umeleta manufaa makubwa kwa wanafunzi chuoni hapo,kwa kuwa wanafunzi wamejifunza Teknolojia mpya kupitia Ujenzi huo kutoka nchini Austria.






📍Ni baada ya MwanaFA kutoa fedha za kugharamia matibabu hayo


MUHEZA:

MBUNGE wa Muheza na Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Hamis Mwinjuma, maarufu kama 'MwanaFA', ametekeleza ahadi yake kwa kutoa chupa 99 za dawa ya kutibu sumu ya nyoka (antivenom) zenye thamani ya shilingi milioni 15, ili ziweze kutolewa bure kwa wananchi.

Mhe. Mwinjuma amekabidhi dawa hizo Julai 24, wakati wa kikao cha ndani cha wana CCM wa Kata za Tongwe na Nkumba, na kueleza kuwa hatua hiyo ni utekelezaji wa ahadi aliyoitoa wakati wa kampeni mwaka jana.

"Mganga Mkuu, niliahidi kwamba endapo wananchi wa Muheza watanichagua tena, dawa za sumu ya nyoka nitazitoa ili wananchi watibiwe bure. Leo nakukabidhi chupa hizi 99 zenye thamani ya shilingi milioni 15," alisema Mhe. Mwinjuma.

Wilaya ya Muheza, yenye jumla ya vijiji 126 na kata 37, imezungukwa na mazingira ya misitu ambayo hupelekea wananchi kung'atwa na nyoka mara kwa mara wanapokuwa katika shughuli zao za mashambani.

Akithibitisha ukubwa wa tatizo hilo wakati akipokea dawa hizo, Mganga Mkuu wa Wilaya ya Muheza, Dkt. Fani Mussa, alisema kwa mwaka 2024/25 pekee, jumla ya watu 108 waliripotiwa kung'atwa na nyoka, huku watu 13 kati yao wakifariki dunia.

"Tunakushukuru mbunge kwa dawa hizi, umewasaidia sana wananchi wetu hapa wilayani kufuatia kilio chao cha muda mrefu. Tutazisambaza katika vituo vyetu vya afya na zahanati na wananchi watakaoumwa na nyoka watatibiwa bure kuanzia sasa," alisema Dkt. Fani.

Inaelezwa kuwa dozi moja ya dawa hiyo inagharimu kati ya shilingi 293,000 hadi 300,000, kiwango ambacho ni kikubwa kwa wananchi wengi wa kawaida kuweza kikumudu kutokana na ugumu huo, waathirika wengi walikuwa wakilazimika kukimbilia kwa waganga wa kienyeji.

Akizungumzia msaada huo, Katibu wa CCM Wilaya ya Muheza, Simon Leng'ese, alimshukuru mbunge huyo na kumwelezea kama kiongozi mwenye utu na anayejali maisha ya wapiga kura wake.

"Mheshimiwa mbunge, kwa niaba ya CCM tunakupongeza sana. Si watu wote wenye moyo kama huo, lakini kwa kitendo hiki cha kutoa dawa, umetenda jambo kubwa ambalo Mungu tu atakulipa. Sisi wenzako wa Muheza tutahakikisha tunakuunga mkono kwa sababu wewe ni hazina ya Muheza na Taifa kwa ujumla," alisema Leng'ese.

Kwa upande wake, mmoja wa wananchi kutoka Kijiji cha Nkumba Stuart Mdachi aliyehudhuria kikao hicho, alipongeza hatua hiyo na kukiri kuwa imekuja wakati mwafaka.

"Kiukweli mbunge tuliyenaye, hiki alichofanya ni jambo kubwa sana. Wananchi wengi walikuwa wakishindwa kwenda hospitali kwa sababu walikuwa hawana shilingi laki tatu, hivyo wanaenda kwa waganga wa kienyeji au kutumia dawa za mitishamba na wakati mwingine kupoteza maisha," alisema mwananchi huyo.






Rais wa IPU afuata nyayo za kiongozi mashuhuri wa Afrika katika ziara yake rasmi ya kikazi nchini Burkina Faso, Rais wa Umoja wa Mabunge Duniani (IPU) Mhe. Dkt. Tulia Ackson ametembelea na kujionea Kituo cha Kumbukumbu cha Thomas Sankara akiambatana na Naibu Spika wa Bunge la Burkina Faso Mhe. Haoua Fofana pamoja na wajumbe wa wabunge.

Wakati wa ziara hiyo, Rais wa IPU ametembelea maeneo mbalimbali ya kituo hicho na kuona alama zinazoakisi safari, misingi ya mawazo na dhamira ya Kapteni Thomas Sankara katika kuwakomboa watu wake na bara la Afrika.

Waongoza wageni wametoa maelezo ya kina kuhusu hatua muhimu za maisha ya Thomas Sankara mazingira yaliyochochea harakati zake za kisiasa na athari endelevu za urithi wake, maelezo hayo yameupa wajumbe hao uelewa mpana zaidi wa historia inayomzunguka shujaa huyo wa Burkina Faso.

Akiwa ameguswa sana kihisia, Dkt. Tulia Ackson ameeleza kuwa ni heshima kubwa kuwepo katika eneo lenye historia nzito na muhimu, amebainisha kuwa ingawa historia ya Thomas Sankara inajulikana sana kupitia vitabu, majarida na vyombo vya habari, kuishuhudia ana kwa ana kunaleta hisia za kipekee.

Ziara hii katika kituo cha kumbukumbu cha Thomas Sankara imempa Rais wa IPU Mhe. Dkt. Tulia Ackson uelewa bora zaidi wa nafasi ambayo Kapteni Thomas Sankara anaendelea kuwa nayo katika kumbukumbu za watu iwe ni nchini Burkina Faso au kimataifa.










Top News