Mameneja wa Kanda na Mikoa wa Taasisi za Shirika la Viwango Tanzania (TBS), Tume ya Ushindani (FCC) pamoja na Wakala wa Vipimo Tanzania (WMA) wameagizwa kuhakikisha hakuna bidhaa bandia na duni katika maeneo yao wanayoyasimamia kiutendaji.

Maelekezo hayo yametolewa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara, Mhe. Balozi Waziri Rajab Salum, wakati wa kikao cha menejimenti za Tume ya Ushindani (FCC), Shirika la Viwango Tanzania (TBS) pamoja na Wakala wa Vipimo Tanzania (WMA), Agosti 21, 2026 jijini Dodoma, kwa lengo la kujadili na kupanga mikakati ya kuimarisha udhibiti wa bidhaa bandia nchini.

Katika kikao hicho, Balozi Salum amesisitiza umuhimu wa taasisi hizo kufanya kazi kwa ushirikiano, weledi, haki na uwajibikaji, akieleza kuwa uratibu mzuri ni muhimu katika kuhakikisha bidhaa zisizokidhi viwango na bidhaa bandia hazitawali soko.

Amesema udhibiti wa bidhaa bandia ni suala muhimu katika kulinda mlaji, wafanyabiashara wanaofuata sheria pamoja na uchumi wa nchi, hivyo taasisi zenye dhamana ya kusimamia soko zinapaswa kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi na kwa kuzingatia sheria na taratibu zilizowekwa.

Balozi Salum amezitaka FCC, TBS na WMA kuongeza ushirikiano katika kubadilishana taarifa, kufanya ukaguzi na kuchukua hatua stahiki dhidi ya wanaojihusisha na uzalishaji, uingizaji au usambazaji wa bidhaa bandia na zisizokidhi viwango.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa watumishi wa taasisi hizo kuwa waadilifu na kutekeleza majukumu yao kwa haki, ili kuhakikisha wafanyabiashara wanafuata sheria wanapata mazingira sawa ya ushindani na walaji wanapata bidhaa salama na zenye ubora.

Amesema matumizi ya teknolojia na taarifa sahihi yanapaswa kupewa kipaumbele katika kuimarisha mifumo ya udhibiti, kutokana na mabadiliko ya mbinu zinazotumiwa na baadhi ya watu katika kusambaza bidhaa bandia katika masoko.

Kwa upande mwingine, kikao hicho kimekuwa fursa kwa viongozi wa FCC, TBS na WMA kueleza changamoto zinazowakabili katika utekelezaji wa majukumu yao, pamoja na kuweka mikakati ya pamoja ya kuongeza ufanisi katika usimamizi wa soko.

Balozi Salum amesisitiza kuwa Serikali itaendelea kuimarisha ushirikiano kati ya taasisi zake ili kujenga mazingira ya biashara yenye ushindani wa haki, kulinda walaji na kuhakikisha wafanyabiashara wanaofuata sheria wanaendelea kufanya shughuli zao katika mazingira salama na yenye tija.

Kikao hicho ni sehemu ya jitihada za Wizara ya Viwanda na Biashara kuimarisha uratibu wa taasisi zake na kuhakikisha majukumu ya udhibiti wa soko yanatekelezwa kwa weledi, haki, uwajibikaji na kwa kuzingatia maslahi mapana ya Taifa.





Maafisa Wakaguzi na Askari wa intake ya 20211/2012 maarufu kwa jina GH Tanzania wanatarajia kuadhimisha miaka 15 ya utumishi wao kazini katika hafla ambayo itakayofanyika Jumamosi, Agosti 22, 2026, katika Shule ya Msingi Mitindo, Misungwi mkoani Mwanza.

Maadhimisho hayo yanatarajiwa kuwa sehemu muhimu ya kutathmini safari ya miaka 15 ya utumishi, huku yakilenga kuimarisha mshikamano, upendo na kujitolea katika kutekeleza majukumu ya kuwahudumia wananchi na jamii kwa ujumla.

Mgeni rasmi katika maadhimisho hayo anatarajiwa kuwa Kamishna wa Kamisheni ya Polisi jamii (CP) Alex Mkama, ambaye ataongoza shughuli mbalimbali zitakazofanyika katika hafla hiyo.

Maadhimisho hayo yamebeba kaulimbiu isemayo “THE HEART OF LOVE”, yenye maana ya “MOYO WA UPENDO”, inayosisitiza umuhimu wa upendo, mshikamano, umoja na kujitolea katika utumishi.

Kwa miaka 15, Maafisa Wakaguzi na Askari wa vyeo mbalimbali wamekuwa sehemu ya safari ya utumishi iliyojaa nidhamu, uwajibikaji, uzalendo na kujitoa katika kutekeleza majukumu yao kwa jamii inayolitegemea Jeshi hilo katika ulinzi na mali zao.

Hafla hiyo inatarajiwa pia kutoa fursa ya kuwakumbusha wahudhuriaji umuhimu wa kuendeleza maadili mema ya utumishi, kusaidiana na kuweka mbele maslahi ya jamii.



 



Na Mwandishi Wetu - Dar es Salaam


Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki, ametoa maelekezo manne kwa Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL), akilitaka kuhakikisha Awamu ya Pili ya Mradi wa Faiba Mlangoni Kwako (Fiber to the Home – FTTH) inawanufaisha wananchi kwa kuwapatia huduma yenye ubora, uhakika na gharama nafuu.

Waziri Kairuki ametoa maelekezo hayo Agosti 21,2026, wakati akizindua rasmi utekelezaji wa Awamu ya Pili ya mradi huo katika Ukumbi wa Johari Rotana, Dar es Salaam, akisisitiza kuwa mafanikio ya mradi hayapaswi kupimwa kwa idadi ya Home Pass au miundombinu iliyojengwa pekee, bali kwa idadi ya wateja wanaounganishwa, ubora wa huduma, kasi ya intaneti na kuridhika kwa wateja.

Ametaka TTCL kupanua wigo wa huduma ya faiba kwa kuhakikisha inafika katika maeneo yenye makazi yanayokua, masoko, maeneo ya biashara, viwanda, shule, vyuo, vituo vya afya na ofisi za Serikali Tanzania Bara na Zanzibar.

Pili, ameitaka TTCL kudumisha ubora wa huduma na kuimarisha huduma kwa wateja, ikiwemo kuhakikisha malalamiko yanashughulikiwa kwa haraka na kwa ufanisi.

Tatu, Waziri Kairuki amelitaka Shirika kuhakikisha huduma hiyo inapatikana kwa gharama nafuu kwa kuandaa vifurushi vinavyokidhi uwezo wa familia, wanafunzi, vijana na wafanyabiashara wadogo na wa kati.

Nne, amesisitiza uwajibikaji na nidhamu ya kibiashara katika usimamizi wa mradi, akitaka wazabuni na wakandarasi wasimamiwe kwa ufanisi ili kazi zikamilike kwa wakati, kwa ubora na kwa kuzingatia thamani ya fedha inayowekezwa.

Waziri Kairuki amesema Mradi wa Faiba Mlangoni Kwako si ujenzi wa miundombinu ya mawasiliano pekee, bali ni hatua ya kimkakati ya kufungua fursa za elimu, biashara, ajira na ubunifu, sambamba na kuchochea ujenzi wa uchumi wa kidijitali nchini.

Amesema mradi huo unaendana na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 na Mkakati wa Taifa wa Uchumi wa Kidijitali 2024–2034, unaolenga kuongeza matumizi ya teknolojia na upatikanaji wa huduma za Serikali kwa njia ya kidijitali.

Kwa mujibu wa Waziri Kairuki, Lengo Namba Nne la Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 linakusudia kuhakikisha ifikapo mwaka 2050 angalau asilimia 70 ya wananchi wanatumia TEHAMA, huku zaidi ya asilimia 80 ya huduma za Serikali zikipatikana kwa njia ya kidijitali iliyo salama na jumuishi.

Akitumia takwimu za Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) kwa robo mwaka iliyoishia Juni 2026, Waziri Kairuki amesema usajili wa intaneti nchini umefikia 62,793,986, huku matumizi ya data yakifikia Petabaiti 1,041.

Hata hivyo, amesema usajili wa huduma ya Faiba Nyumbani ulikuwa 178,904, hali inayoonyesha kuwa bado kuna fursa kubwa ya kukuza huduma ya intaneti ya kasi kupitia teknolojia ya nyuzi za macho.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi Mkuu wa TTCL, CPA Moremi Marwa, amesema Awamu ya Pili ya Mradi wa Faiba Mlangoni Kwako ni sehemu ya utekelezaji wa Mpango Mkakati wa Biashara wa Miaka 10 wa Shirika kwa kipindi cha 2025/26 hadi 2034/35, unaolenga kuimarisha na kuboresha huduma za mawasiliano nchini.

Marwa amesema TTCL imeingia katika Awamu ya Pili ikiwa tayari imejenga msingi muhimu kupitia utekelezaji wa Awamu ya Kwanza, iliyolenga maeneo mbalimbali ya kimkakati nchini.

Amesema katika Awamu ya Kwanza, TTCL imefanikiwa kujenga zaidi ya Home Pass 280,000, huku jumla ya maungio ya huduma ya nyuzi za macho yakifikia karibu 300,000 nchini.

Kwa upande wa Awamu ya Pili, amesema TTCL inalenga kuongeza zaidi ya Home Pass 400,000, hatua inayotarajiwa kupanua wigo wa upatikanaji wa intaneti ya kasi kwa wananchi, taasisi na wafanyabiashara.

Marwa amesema TTCL katika utekelezaji wa Awamu ya Pili imeendelea kutumia teknolojia ya kisasa ya Gigabit Passive Optical Network (GPON) badala ya mfumo wa Point-to-Point uliokuwa ukitumika awali.

Amesema teknolojia hiyo inawezesha TTCL kuwahudumia wateja wengi kwa wakati mmoja, kuongeza ufanisi wa matumizi ya miundombinu, kupunguza gharama za uendeshaji na kuboresha ubora wa huduma za intaneti.

Ameongeza kuwa matumizi ya teknolojia hiyo yanaipa TTCL uwezo wa kutumia miundombinu ya nyuzi za macho kwa ufanisi zaidi na kuongeza uwezo wa kutoa huduma ya intaneti yenye kasi na uhakika kwa watumiaji.

Mkurugenzi Mkuu huyo amesema utekelezaji wa mradi huo unafanyika kwa ushirikiano na makandarasi wa ndani na wa kimataifa, wakiwemo Huawei, ZTT na Visoll, katika ujenzi na uendelezaji wa miundombinu ya nyuzi za macho.

Amesema ushirikiano huo ni sehemu ya jitihada za kuhakikisha upanuzi wa mtandao unafanyika kwa kutumia teknolojia za kisasa na kukidhi mahitaji yanayoongezeka ya huduma za intaneti nchini.

Marwa amesema Awamu ya Kwanza ya Mradi wa Faiba Mlangoni Kwako ililenga maeneo mbalimbali ya kimkakati, ikiwemo Dar es Salaam, Arusha, Dodoma, Geita, Iringa, Mbeya na Mwanza, pamoja na Unguja, Zanzibar.

Amesema mafanikio yaliyopatikana katika awamu hiyo yameiwezesha TTCL kuendelea na upanuzi wa miundombinu kupitia Awamu ya Pili, huku ikilenga kuwafikia wananchi wengi zaidi.

Mradi huo unalenga pia kuchochea matumizi ya teknolojia katika shughuli za kila siku, biashara, elimu na huduma za Serikali, sambamba na kuongeza fursa za kiuchumi kupitia upatikanaji wa intaneti yenye kasi na uhakika.

Waziri Kairuki amewataka wananchi kutumia fursa hiyo katika kujifunza, kufanya biashara, kuongeza uzalishaji, kubuni fursa mpya za ajira na kupata huduma za Serikali kwa njia ya kidijitali.

Aidha, amewataka wananchi kushirikiana na Serikali katika kulinda miundombinu ya mawasiliano dhidi ya uharibifu na wizi, ili kuhakikisha uwekezaji huo unaendelea kutoa huduma bora na kuchangia maendeleo ya uchumi wa kidijitali nchini.





 




Na Oscar Assenga, MUHEZA

MKUU wa Mkoa wa Tanga, Balozi Dkt. Batilda Burian, amewataka wananchi 66 wa Kitongoji cha Bago Maisha Plus ,Kijiji cha Msakangoto, Kata ya Kigombe wilayani Muheza, kuondoka katika eneo walilokuwa wakiishi na kuhamia eneo jipya lililotengwa na Serikali ya Kijiji, huku akiahidi kuwa Serikali itaendelea kuwasaidia katika kipindi cha mpito.

Wananchi hao wamekumbwa na changamoto hiyo baada ya nyumba zao kubomolewa kufuatia utekelezaji wa amri ya mahakama iliyotokana na mgogoro wa umiliki wa eneo hilo.

Balozi Burian alitoa kauli hiyo leo alipofanya ziara katika eneo hilo na kukutana na wananchi hao, ambapo alisema Serikali haina mamlaka ya kuzuia utekelezaji wa amri ya mahakama.

Alisema baada ya kubaini kuwa eneo hilo lilikuwa ndani ya hati ya umiliki ya mwekezaji wa Mashamba ya Mkonge ambaye tayari alikuwa amefungua kesi mahakamani na kupata amri ya kuwaondoa wananchi, Serikali ililazimika kuheshimu uamuzi huo.

“Serikali haiwezi kupingana na sheria ya mahakama. Aliyekuja kubomoa alikuwa anatekeleza maelekezo ya mahakama. Hata hivyo, sisi kama Serikali tuliona ni lazima tuzungumze na wananchi na mwekezaji ili kutafuta suluhisho la kibinadamu,” alisema.

Alisema awali wananchi hao walipelekwa katika eneo hilo na Serikali ya Kijiji, huku wakiwa na vielelezo vilivyoonyesha kuwa waliruhusiwa kuishi katika eneo hilo, jambo lililopelekea Serikali ya Mkoa kuingilia kati baada ya mgogoro kujitokeza.

Balozi Burian alisema Serikali ya Mkoa imefanya mazungumzo na mwekezaji kupitia Wizara inayohusika na Uwekezaji, hatua iliyosaidia kuwezesha kupatikana kwa eneo jingine kwa ajili ya kuwahamishia wananchi hao.

Alisema eneo lililotengwa awali kwa ajili ya makazi mapya lilibainika kuwa halifai kutokana na kuwa na maji, hivyo Serikali ililazimika kutafuta eneo jingine.

“Wawakilishi wenu wamekuja ofisini kwangu mara tatu. Hatua ya kwanza ilikuwa kwenda kuzungumza na mwekezaji, hatua ya pili mwekezaji akakubali kutoa Sh200,000 na hatua nyingine ni kuhakikisha hakuna mtu anayewasumbua wakati taratibu za kuwahamisha zikikamilishwa,” alisema.


Balozi Burian alisema maturubai  ambayo  wanayatumia kwa  muda wakati wakijiandaa kujenga makazi yao mapya.

“Kesho asubuhi tutahamisha maturubai hayo kwenda kwenye eneo ambalo mtaenda kuhamia. Mtayatumia kwa mwezi mmoja wakati mkiendelea kujipanga kujenga makazi yenu,” alisema.

Alisema Serikali itaendelea kutafuta wadau na wasamaria wema watakaoweza kusaidia katika ujenzi wa makazi mapya kwa wananchi hao.

Aidha, aliwataka wananchi hao kutokata tamaa na kuacha kuchukua hatua zinazoweza kuwaingiza katika mgogoro mwingine wa kisheria.

“Ndugu zangu, mchakato mzima nimewaeleza. Sina mamlaka ya juu zaidi ya hapa. Kila mhimili una kiwango chake cha kushughulikia jambo. Likishafika mahakamani, Serikali haiingilii tena,” alisema.

Alisema wananchi wanapaswa kuanza maisha katika eneo jipya huku wakiamini kuwa Serikali itaendelea kushirikiana nao katika kutafuta suluhisho la changamoto zinazowakabili.

Akizungumza kwa niaba ya wananchi hao, Ally Mohamed, mkazi wa Maisha Plus, alisema suala la fidia limekuwa miongoni mwa changamoto kubwa zilizowafanya kuwa na wasiwasi kuhusu kuhamia eneo jipya.

Alisema baadhi yao walitumia mafao waliyopata kutoka Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) kujenga nyumba zao, hivyo kubomolewa kwa nyumba hizo kumewasababishia hasara kubwa.

“Baadhi yetu tulitumia mafao yetu ya NSSF kujenga nyumba. Sasa nyumba zimebomolewa na tunajiuliza tutaanzaje maisha upya,” alisema.

Akijibu suala hilo, Balozi Burian alisema wananchi waliokuwa na madai ya fidia wakati shauri likiendelea walikuwa na nafasi ya kuyawasilisha mahakamani.

Hata hivyo, alisema Serikali ya Mkoa imeendelea kufanya mazungumzo na mwekezaji kwa lengo la kutafuta namna ya kuwasaidia wananchi hao katika kipindi hiki cha mpito.


Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Kigombe (CCM) Shahongwe Mgandi aliishukuru Serikali ya Mkoa kwa hatua iliyochukua, akisema viongozi wa kata watahakikisha wananchi hao wanapata usalama na huduma muhimu katika eneo jipya.

Alisema Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) limeanza maandalizi ya kufikisha huduma ya umeme katika eneo hilo, ikiwa ni pamoja na kusimika nguzo.

Alisema pia maeneo ambayo wananchi hao watahamia yatatambuliwa kisheria na kutambuliwa kama kitongoji, huku Serikali ikiendelea kuboresha barabara na huduma nyingine muhimu.

Mwenyekiti wa Kijiji cha Maisha Plus alishukuru Serikali ya Mkoa kwa hatua hiyo na kuiomba iruhusu wananchi hao, inapowezekana, kuhamisha baadhi ya miti waliyokwishaipanda katika eneo la awali ili kuitumia katika mazingira ya makazi mapya.

Hatua hiyo, alisema, itawasaidia wananchi hao kuanza maisha mapya huku wakitunza mazingira katika eneo watakalohamia.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Dkt. Mahmoud Thabit Kombo (Mb), amepokea Nakala za Hati za Utambulisho kutoka kwa Balozi Mteule wa Ubelgiji nchini Tanzania, Mhe. Lot Debruyne, katika Ofisi Ndogo za Wizara, jijini Dar es Salaam.

Baada ya makabidhiano hayo, viongozi hao wamejadili namna ya kuendelea kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia na ushirikiano kati ya Tanzania na Ubelgiji, huku wakisisitiza umuhimu wa kukuza biashara na uwekezaji.

Akizungumza na Balozi Mteule huyo, Waziri Kombo amesema Tanzania inalenga kuhamisha mwelekeo wa ushirikiano kutoka katika utegemezi wa misaada na kuelekea katika biashara na uwekezaji wenye manufaa kwa pande zote.

Ametaja kilimo na umwagiliaji, uhamishaji wa maarifa na ujuzi, pamoja na upatikanaji wa mitambo na teknolojia za kisasa za kilimo kuwa miongoni mwa maeneo yenye fursa kubwa za ushirikiano.

Aidha, Waziri Kombo amesisitiza umuhimu wa kuongeza biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na Ubelgiji, akieleza kuwa ongezeko la watalii kupitia safari za moja kwa moja za Brussels Airlines kwenda Kilimanjaro na Zanzibar ni fursa muhimu ya kukuza sekta ya utalii.

Viongozi hao pia wamebainisha maeneo mengine ya ushirikiano, ikiwemo ustahimilivu dhidi ya mabadiliko ya tabianchi, nishati safi na jadidifu, nishati ya kupikia safi, mabadiliko ya kidijitali na afya.

Kwa upande mwingine, wamejadili umuhimu wa kuimarisha ushirikiano kati ya Bandari za Antwerpen nchini Ubelgiji na Dar es Salaam, pamoja na fursa za ushirikiano kati ya Chuo Kikuu cha Ghent na taasisi za elimu nchini Tanzania katika kukuza matumizi na ufundishaji wa lugha ya Kiswahili.








Top News