Na Mwandishi Wetu

WANAWAKE watatu wamebahatika kupata fursa ya kupandikiza mimba bure katika kituo cha kupandikiza mimba cha Kairuki Green IVF (KGIVF), Kilichoko Bunju A Mianzini jijini Dar es Salaam.

Walipata fursa hiyo jana jioni wakati wa droo iliyochezeshwa na mgeni rasmi Jokate Mwegelo wakati wa sherehe za siku ya wanawake zilizoandaliwa na Mtandao wa Elimu ya Afya Kairuki (KHEN) jijini Dar es Salaam .

Wanawake hao ni miongoni mwa wanawake zaidi ya 137 wa mikoa mbalimbali walioomba kupata fursa hiyo ya bure lakini katika mchujo uliofanyika walibahatika wanawake hao watatu pekee.

Kwa wastani gharama za kupandikiza mimba kwa Tanzania ni kati ya shilingi milioni 18 mpaka 20.

Mkurugenzi wa KGIVF, Dk Clementina Kairuki alisema waliopata fursa hiyo watahudumiwa bure kuanzia hatua za awali hadi kupandikiza mimba kama sehemu ya kituo hicho kusaidia jamii.

Alisema wameamua kutoa huduma hiyo bure kama sehemu ya kusherehekea siku ya mwanamke duniani kuwapa furaha ya kupata familia wanawake ambao wamekuwa wakitamani kupata familia lakini wanashindwa kutokana na kukosa pesa.

Alisema KGIVF iliona wanawake wengi wamekuwa wakijitokeza kutaka kupandikizwa mimba kwenye kituo hicho lakini asilimia 30 hawawezi kumudu gharama za huduma hiyo.

“Kuna watu wengi wanapata shida wanatukanwa kwenye familia wanaachika kwenye ndoa kwasababu hawajabahatika kupata watoto, tafiti zinaonyesha kuwa kila ndoa sita moja inachangamoto ya kupata watoto ndiyo maana tukaona tutoe fursa hii,” alisema

Alisema KGIVF imekuwa ikitoa elimu kwa jamii kuhusu ukubwa wa tatizo hilo na namna bora ya kupata suluhu ya kulitatua kwa kupandikiza mimba.

“Tumetambua kuwa kuna watanzania wengi wenye tatizo hili lakini hawana uwezo wa kuja KGIVF kupandikiza mimba kwasababu ya uwezo wa kifedha ndiyo maana tumechagua wanawake watatu tuwape huduma hii bure kama sehemu ya kutoa elimu kwa jamii,” alisema

Mgeni rasmi kwenye hafla hiyo, Jokate Mwegelo alisema Mtandao wa Elimu ya Afya Kairuki (KHEN) ni mfano wa kuigwa ukanda wa Afrika Mashariki na Kati kutokana na mambo makubwa waliyofanya.

Alisema KHEN imefanya mambo makubwa ikiwemo kuanzisha Kituo cha kupandikiza mimba KGIVF, Kairuki Hospitali, Kiwanda cha kutengeneza dawa kilichoko Kibaha mkoani Pwani, Chuo Kikuu Kairuki na Kampasi ya chuo hicho iliyoko Boko.

“Mimi ni mdau mkubwa sana wa Kairuki, nimekuwa nikiwasemea sana na leo naomba nijirasimishe kuwa balozi wa Kairuki, nitawasemea vizuri popote nitakapokuwa kwasababu nyinyi mmeonyesha mfano wa kuigwa kwenye kusaidia jamii yetu,” alisema Jokate Mwegelo.

“Mimi nitakuwa balozi wa viwango kwasababu nimeona Kairuki ni taasisi ya viwango vya juu sana, siongei haya kumfurahisha mtu hapa nasema hili kutoka kwenye sakafu ya moyo wangu, katika taasisi zilizoasisiwa na watanzania wenzetu, Kairuki ni taasisi ya mfano Afrika Mashariki na Kati kwasababu imesimama na haitetereki,” alisema

“Wako watu walianzisha biashara hata miaka mitatu haijafika zikafa, lakini leo hii ukizungumzia Kairuki unazungumzia Hospitali, unazungumzia Kairuki Green IVF, unazungumzia kiwanda cha dawa Kibaha, chuo cha Kairuki ambacho kinawanafunzi zaidi ya 2,000 nani kama Kairuki,” alisema




















📌 Umeme umewashwa kwa mara ya kwanza katika vitongoji viwili

📌 Zaidi ya Shilingi bilioni 60 zatumika kusambaza umeme kwenye vitongoji vya mkoa wa Shinyanga


Kahama, Shinyanga📍

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imeridhishwa na namna fedha za Bajeti ya Mwaka 2025/2026 zilizoidhinishwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania zinavyotumika katika utekelezaji wa Miradi ya kusambaza umeme kwenye vitongoji kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA).

Akizungumza wakati wa ziara ya Kamati pamoja na zoezi la kuwasha umeme kwa mara ya kwanza katika kitongoji cha Mine, kata ya Mwakata, Jimbo la Msalala na kitongoji cha Mjimwema katika Jimbo la Kahama wilaya ya Kahama mkoani Shinyanga, Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Subira Mgalu, amesema ziara ya kamati imelenga kukagua na kujionea utekelezaji wa Miradi ili kuhakikisha fedha zilizotengwa na Bunge zinatumika kwa ufanisi.

“Tumepewa dhamana na Bunge kuhakikisha fedha zilizotengwa zinatekeleza kusudi lililokusudiwa. Bunge lilitenga bajeti ya shilingi bilioni 400 kwa mwaka wa fedha 2025/2026 kwa ajili ya miradi ya kufikisha umeme vitongojini, na tumekuja kuona thamani ya fedha hizo kama imetumika ipasavyo. Kwa kweli tumeridhishwa na kazi inayofanywa na REA,” amesema Mhe. Mgalu.

Ameongeza kuwa utekelezaji wa miradi hiyo unaonesha mafanikio makubwa ya Serikali ya Awamu ya Sita ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, inayoongozwa na  Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuhakikisha wananchi wa vijijini wanapata huduma ya umeme.

Naye Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba, amesema ukaguzi wa miradi unaofanywa na Kamati ya Bunge ni sehemu muhimu ya utekelezaji wa Katiba, inayolenga kuhakikisha Bunge linasimamia ipasavyo matumizi ya fedha za umma katika miradi ya maendeleo.

Makamba amesema katika bajeti ya Wizara ya Nishati, ilipanga kuwa kila jimbo nchini litapatiwa vitongoji 15 vitakavyofikishiwa huduma ya umeme ili kuongeza kasi ya maendeleo kwa Wananchi.

Amesema Miradi hiyo inaendelea kubadilisha maisha ya Wananchi kwa kuchochea shughuli za kiuchumi pamoja na kuboresha huduma za kijamii na kuongeza fursa za maendeleo katika maeneo ya vijijini.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Umeme Vijijini kutoka REA, Mhandisi Jones Olotu aliyemwakilisha Mkurugenzi Mkuu wa taasisi hiyo, amesema mkoa wa Shinyanga una jumla ya vitongoji 2,704 ambapo kati ya hivyo vitongoji 1,180 tayari vimefikishiwa huduma ya umeme.

Amesema vitongoji 582 vipo katika Mradi wa HEP II (B); Mradi uliosainiwa Januari mwaka huu ambao unatarajiwa kukamilika ndani ya kipindi cha miaka mitatu.

“Kuanzia mwaka wa fedha 2024/2025 hadi sasa REA imeidhinisha zaidi ya shilingi bilioni 61 kwa ajili ya kufikisha umeme katika vitongoji mbalimbali vya mkoa wa Shinyanga,” amesema Mhandisi, Olotu.

Aidha ameahidi kuwa REA itaendelea kutekeleza maelekezo ya Serikali na Bunge kuhakikisha ifikapo mwaka 2030 vitongoji vyote nchini vinafikiwa na huduma ya umeme.









Kamati ya Bunge ya Kudumu ya Miundombinu ikipata maelezo kutoka kwa Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Reli Tanzania (TRC) Mhandisi Mhandisi Machibya Shiwa wakati Kamati hiyo ilipotembelea na kukagua mradi wa uundaji wa vichwa vya Treni za MGR  unaoendelea katika Karakana ya Pugu jijini Dar es Salaam.

Kamati ya Bunge ya Kudumu ya Miundombinu ikwa katika moja ya kichwa katika kilichoundwa  wakati walipotembelea na kukagua mradi wa uundaji wa vichwa vya Treni za MGR  unaoendelea katika Karakana ya Pugu jijini Dar es Salaam.
Kichwa cha Treni za MGR kilichoundwa katika Karakana ya Pugu jijini Dar es Salaam.

*Tanzania yawa nchi ya kwanza katika ukanda wa Afrika Mashariki

Na Mwandishi Wetu 

Kamati ya Bunge ya  Kudumu ya Miundombinu, imelitolea wito Shirika la Reli Tanzania (TRC) kuendelea kuwajengea uwezo vijana wa Kitanzania wanaounda na kukarabati vichwa vya treni za MGR, kwa kuwapa mafunzo thabiti ndani na nje ya nchi ili kuongeza maarifa, stadi na ubunifu katika utendaji wao kazi hiyo  .

Hayo ameyasema  Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya  Kudumu ya Miundombinu  Selemani Kakoso,  wakati wa ziara ya kamati hiyo iliyolenga kukagua mradi wa uundaji wa vichwa vya treni za MGR, unaoendelea katika karakana ya Pugu, Jijini Dar es Salaam. 

Kakoso kwa niaba ya kamati hiyo, ameitaka TRC kuhakikisha  inawapa fursa na kuwapeleka vijana hao wenye ujuzi nje ya nchi kujifunza  na kuchota utalaamu zaidi ili kuongeza ufanisi katika utendaji wao, aidha alitoa rai kwa TRC  kuwapa k kipaumbele katika suala la ajira  ili waendelee kulitumikia shirika na nchi kwa uaminifu.

Aidha Kakoso, alisema kamati inaipongeza kwa dhati  TRC na Mkurugenzi wake Mkuu Mhandisi Machibya Shiwa, ambapo  kwa mara ya kwanza katika historia, Tanzania  imefanikiwa kufanya hivyo kufuatia ucheleweshwaji wa vipuri kimkataba kutoka kwa wazabuni wa vipuri wa SMH Kutokana vita kati ya Ukraine na Urusi, hivyo TRC ilifanya maamuzi ya kusafirisha vichwa viwili vilivyokamilika na kuundwa nchini Malaysia na kusafirisha vipuri kutoka kw wazabuni kuja nchini na kuanzaz uundwaji wa vichwa sita vilivyobaki katika karakana ya Pugu.

Kakoso, ameongeza kusema kuwa uamuzi wa TRC kuunda  vichwa vya treni hapa nchini  umepunguza gharama kubwa ambayo serikali ingetumia kuagiza vichwa hivyo na pia imewezesha vijana wengi wa Kitanzania wenye ujuzi kuajiriwa aidha Mhe. Kakoso amewaasa watumishi wa Shirika la Reli Tanzania kuwa wazalendo katika kulitumikia Shirika na kutunza rasilimali zilizopo na kuepuka vitendo vya hujuma kwa  shirika.

Katika hatua nyingine, Naibu Waziri wa Wizara ya Uchukuzi Mhe.David Kihenzile, ameendelea kuipongeza Serikali kupitia TRC kwa kukuza sekta ya uchukuzi kwa kuendelea kujenga  miundombinu bora na yenye ufanisi na kununua vitendea kazi ikiwemo vichwa na behewa.

"Nampongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuboresha sekta ya uchukuzi , serikali imeendelea na ujenzi wa reli ya kisasa zaidi ya kilomita 2290 na sasa inanunua vitendea ili kuboresha sekta hii." alikazia  Mhe.Kihenzile.

Awali Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Reli Tanzania Mhandisi Machibya Shiwa, Pamoja na masuala mengine, aliiambia kamati hiyo ya kudumu ya Bunge ya Miundombinu juu ya manufaa ya mradi wa uundaji wa vichwa vya treni za MGR Daraja la 91XX katika karakana ya Pugu, ni Pamoja na fursa za ajira amabpo jumla ya vijana 34 ambao hawakuwa wameajiriwa sasa wameajiriwa kupitia mradi huo. Aidha Mhandisi Shiwa, alisema, “kupitia mradi huo baadhi ya Watanzania, wamepata kuuza bidhaa zinazotumika katika uundaji wa vichwa hivyo nao ni kama wenye mashine za kuchinga vipuri, wauzaji wa vifaa ujenzi, bolt na nati, wauzaji vifaa vya umeme, mabomba, wauzaji vilainishi, bidhaa za mpira nk’’, alimalizia Mkurugenzi mkuu huyo wa TRC.






Matukio mbalimbali katika picha ya Kamati ya Bunge ya Kudumu ya Miundombinu   ilipotembelea na kukagua mradi wa uundaji wa vichwa vya Treni za MGR  unaoendelea katika Karakana ya Pugu jijini Dar es Salaam.

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Maendeleo ya Uongozi wa Elimu (ADEM), Dkt. Maulid J. Maulid, amefungua kikao kazi cha Chama cha Kulinda na Kutetea Haki za Walimu (CHAKUHAWATA) kinachofanyika jijini Dodoma, akisisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya wadau mbalimbali wa sekta ya elimu ili kuimarisha uongozi, utawala bora na udhibiti wa ubora wa elimu nchini.

Akizungumza katika hafla ya ufunguzi wa kikao hicho, Dkt. Maulid amesema ADEM imekuwa ikifanya kazi kwa karibu na jumuiya mbalimbali za elimu zikiwemo TAHOSSA, TAPSHA na REDEOA pamoja na mashirika ya kitaifa na kimataifa, kwa lengo la kuunganisha nguvu katika kufanikisha malengo ya kitaifa ya maendeleo ya elimu.

Amesema mwaliko wa kushiriki katika kikao hicho muhimu cha wadau wa sekta ya elimu umefungua ukurasa mpya wa ushirikiano kati ya ADEM na CHAKUHAWATA, kwani hapo awali taasisi hizo hazikuwa na ushirikiano wa karibu katika shughuli zao.

“Taasis yetu itaitumia fursa hii na jukwaa hili muhimu kuhakikisha tunafanya kazi kwa karibu kuwajengea uwezo walimu na viongozi wa elimu nchini,” amesema Dkt. Maulid.

Aidha, ameipongeza CHAKUHAWATA kwa juhudi zake za kutekeleza majukumu yake na kwa namna inavyowasaidia wanachama wanaokumbwa na changamoto mbalimbali ikiwemo masuala ya ajira, majanga na ustawi wa walimu.

Dkt. Maulid amesema juhudi hizo zimechangia kukua kwa chama hicho kutoka wanachama 182 wakati wa kuanzishwa kwake mwaka 2015 hadi kufikia wanachama 49,750 kwa sasa.

Amesisitiza pia umuhimu wa kuimarisha mawasiliano kati ya chama hicho na taasisi au wizara zinazowasimamia waajiri wa wanachama wao ili kujenga uelewa wa pamoja na kutatua changamoto zinazojitokeza kwa njia za kisheria na maelewano.

Katika hatua nyingine, amewahimiza viongozi wa CHAKUHAWATA kusimamia matumizi sahihi ya rasilimali za wanachama na kuimarisha ushiriki wa wanachama katika vikao vya chama ili kutoa mawazo yatakayosaidia kukijenga chama kwa mujibu wa katiba yake.

















Top News