
NI miaka 30 tangu kuanzishwa kwa Taasisi ya Saratani nchini Tanzania (Ocean Road). Kuanzishwa kwake kumeleta matumaini ya kuendelea kuishi kwa mamilioni ya wananchi.
Kila safari kubwa huanza na maono, matumaini, ujasiri na imani kwamba hata katika nyakati ngumu maisha yanaweza kulindwa. Mwaka 1996, katika changamoto za kiafya na rasilimali chache, wazo moja lilizaliwa si kwa hofu bali kwa maarifa, huruma na uthubutu.
Haikuwa rahisi kuanza safari hiyo ngumu, lakini taasisi hiyo ilijengwa kwa dhamira thabiti ya kuhudumia watu.
Dkt. Hamza Maunda anasimulia kuwa hali ilikuwa ngumu kwa kuwa taasisi ilianza ikiwa na uhaba wa wafanyakazi na vifaa tiba kwa ajili ya matibabu ya saratani.
“Taasisi hiyo iliendelea kuimarika siku hadi siku mpaka kufikia hatua ya kuwa na wataalamu waliosoma ndani ya taasisi hiyo,” alisema.
“Pamoja na changamoto zote, tuliweza kujijenga siku hadi siku, na mwaka 2013 taasisi ilianzisha masomo ya kuwafundisha madaktari kubobea katika eneo la saratani; hiyo ilikuwa hatua muhimu sana,” aliongeza Dkt. Maunda
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Saratani Ocean Road, Dkt. Diwani Msemo, akieleza mafanikio ya taasisi hiyo amesema yametokana na uwekezaji wa serikali.
“Rais Samia, kwa kipindi cha miaka yake minne ya awamu ya sita, aliwekeza zaidi ya shilingi milioni 40 kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya matibabu ya saratani,” alisema Dkt. Msemo.
Amesema kuwa jitihada za serikali ziliipa nguvu taasisi hiyo, hususan Wizara ya Afya, kuanzisha mpango maalumu wa kushughulikia saratani.
Ameeleza kuwa mafanikio ya Ocean Road yameifanya serikali kuongoza jitihada za makusudi za kuwasogezea wananchi huduma hizo.
“Wananchi walikuwa wakisafiri umbali mrefu, wengine kilometa 1,000 hadi 1,300, kufuata huduma hii. Serikali ikaona iwasogezee wananchi huduma hiyo karibu,” alisema.
Dkt. Yokebeth Vuhahula, daktari bingwa wa saratani, amesema awali taasisi hiyo ilikuwa inategemea wagonjwa kupimwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili kabla ya kupelekwa kutibiwa Ocean Road.
“Tulikuwa hatuna idara ya Patholojia, ambayo ni muhimu sana katika taasisi za saratani kwa maana ndicho kipimo kinachoonesha kama mgonjwa ana saratani. Tulikuwa tunasubiri wagonjwa wapimwe Muhimbili, lakini sasa vipimo vinafanyika hapa,” alisema.
Mwanga Mhoka, mtaalamu wa vipimo vya Patholojia, amesema taasisi hiyo imepiga hatua zinazoonekana kwa macho.
“Tumepiga hatua kubwa; tulikuwa na wauguzi wachache na vifaa vichache, lakini sasa mambo ni mazuri,” alisema.
Dkt. Jasmin Salum ni mmoja wa waliopona saratani baada ya kufika katika taasisi hiyo.
“Nilipoambiwa nina saratani nilijua tayari maisha yameisha, lakini taasisi hii imenirudishia tumaini la kuendelea kuishi,” alisema.
Naye Babu wa Kitaa, mtangazaji wa Clouds Media Group, ni shuhuda wa matibabu ya taasisi hiyo, akiwa ni mmoja wa wagonjwa waliohudumiwa na kupona.
“Kwanza namna nilivyohudumiwa hapa, kuanzia kwa wauguzi mpaka kwa madaktari, ilikuwa huduma nzuri sana, yenye ukarimu na uweledi wa hali ya juu,” alisema.
Babu wa Kitaa amesema kilichompa matumaini zaidi ni kuona watu wengi waliokoa maisha yao katika taasisi hiyo.
“Hapo ndipo nilielewa kuwa Ocean Road ina nafasi kubwa ya kubadilisha maisha ya watu wengi ambao hawana uwezo wa kwenda nje ya nchi kupata matibabu,” alisema.
Ameongeza kuwa kwa sasa nchi jirani zinakimbilia Ocean Road si kwa sababu ya jina, bali kwa sababu ya ubora wa huduma.

































.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)




.jpeg)


