Na Mwandishi Wetu - Zanzibar

Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL) limeendelea kuunga mkono juhudi za Serikali za kujenga mazingira wezeshi kwa uchumi wa kidijitali Zanzibar kwa kuwezesha huduma ya intaneti katika mradi wa makazi wa Amani Residency, uliopo Kizimkazi, Mkoa wa Kusini Unguja, kupitia huduma yake ya Faiba Mlangoni Kwako.

Mradi huo wa kisasa wa makazi ulizinduliwa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, ukiwa ni sehemu ya uwekezaji unaolenga kuongeza fursa za makazi bora, biashara na utalii pamoja na kuchochea shughuli za kiuchumi Zanzibar.

Akizungumza kuhusu uwezeshaji huo, Meneja wa TTCL Zanzibar, Bi. Nasra Mugheiry, alisema TTCL imeweka mazingira ya mawasiliano ya kisasa katika Amani Residency ili kuwawezesha wakazi kupata huduma ya intaneti karibu na makazi yao na kutumia fursa mbalimbali zinazotokana na uchumi wa kidijitali.

“TTCL kupitia huduma ya Faiba Mlangoni Kwako imeweka mazingira wezeshi ya mawasiliano katika Amani Residency, kwa lengo la kuwawezesha wakazi kutumia intaneti katika shughuli zao za kila siku, ikiwemo kazi, biashara, elimu, mawasiliano na huduma mbalimbali za kidijitali. Tunataka kuhakikisha kwamba makazi ya kisasa yanaendana na mahitaji ya kisasa ya mawasiliano,” alisema Bi. Mugheiry.

Huduma hiyo inatarajiwa kuongeza thamani ya mradi huo kwa kuwawezesha wakazi kufanya shughuli mbalimbali kwa urahisi wakiwa majumbani. Kwa wakazi wanaofanya kazi kwa njia ya mtandao, wafanyabiashara, wanafunzi na familia, upatikanaji wa intaneti ya nyumbani utarahisisha matumizi ya mikutano ya mtandaoni, kujifunza, kufanya biashara kupitia majukwaa ya kidijitali, mawasiliano pamoja na huduma za Serikali mtandao.

Amani Residency, unaojengwa katika eneo la ekari 11, una jumla ya nyumba 82, zikiwemo villa 18 na apartment 64, pamoja na huduma mbalimbali za burudani na mapumziko. Uwepo wa huduma ya Faiba Mlangoni Kwako unaifanya miundombinu ya mawasiliano kuwa sehemu muhimu ya mazingira ya makazi hayo, sambamba na mahitaji ya maisha ya kisasa.

Kwa upande wa biashara, intaneti inayopatikana katika makazi inaweza kuwapa wakazi fursa ya kuendesha shughuli zao za kiuchumi kwa kutumia teknolojia, ikiwemo biashara za mtandaoni, masoko ya kidijitali, huduma za kifedha na mawasiliano ya kibiashara. Hali hiyo inaendana na juhudi za TTCL za kuchochea matumizi ya teknolojia na kuunganisha wananchi na fursa za uchumi wa kidijitali.

Aidha, uwezeshaji huo unaimarisha dhamira ya TTCL ya kusogeza huduma za mawasiliano kwa wananchi katika maeneo wanayoishi na kufanya shughuli zao, kwa kuzingatia kwamba intaneti imekuwa sehemu muhimu ya maisha ya kila siku na kichocheo cha maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Kwa TTCL, kuwezesha Amani Residency kwa huduma ya Faiba Mlangoni Kwako ni zaidi ya kuunganisha makazi na intaneti; ni hatua ya kujenga mazingira ambayo yanawawezesha wananchi kuishi, kufanya kazi, kujifunza, kuwasiliana na kufanya biashara kwa kutumia teknolojia, sambamba na juhudi za taifa za kujenga uchumi unaotegemea zaidi huduma na fursa za kidijitali.






Wananchi wa Mkoa wa Tanga na mikoa jirani wanahamasishwa kushiriki katika Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ubunifu na Ujuzi, itakayofanyika kuanzia tarehe 15 - 24 Agosti 2026 katika viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara, jijini Tanga, ili kujifunza, kubadilishana maarifa na kutumia fursa mbalimbali za elimu, ujuzi na ubunifu.

Akizungumza Agosti 14, 2026, Katibu Tawala wa Mkoa wa Tanga, Rashid Kassim Mchata, amesema maonyesho hayo yatashirikisha taasisi zaidi ya 300 pamoja na wadau wa sekta ya elimu, sayansi na teknolojia. Aidha, kutakuwa na mashindano ya ubunifu na ujuzi katika fani mbalimbali ikiwemo ushonaji, ususi, umeme na mengineyo, ambapo washindi wa kitaifa watapata nafasi ya kushiriki mashindano ya kimataifa.

Mchata ameongeza kuwa wadhamini mbalimbali wakiwemo mabenki wamejitokeza kudhamini miradi ya ubunifu na kuunga mkono wajasiriamali chipukizi.

Kwa upande wake, Prof. Ladislaus Mnyone, Mkurugenzi wa Idara ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu, alisema lengo kuu la wiki hiyo ni kuwaleta pamoja wadau kujadili na kuweka mikakati ya pamoja kuhusu elimu, ujuzi na ubunifu.

Amebainisha kuwa matukio makuu yatakuwa ni maonesho ya teknolojia yanayoonyesha mchango wa sayansi katika sekta mbalimbali, pamoja na kongamano la elimu na ubunifu litakalojadili utekelezaji wa Dira 2050.

Prof. Mnyone amefafanua kuwa kongamano hilo litaangazia nyenzo tano kuu: utafiti na maendeleo, sayansi na ubunifu, teknolojia za kidijitali, nishati, na usafirishaji funganishi.

Kupitia mijadala na maonesho hayo, Wizara inalenga kufanikisha malengo ya taifa ikiwemo kufikia uchumi wa dola trilioni 1 ifikapo mwaka 2050, kipato cha wastani cha mtu mmoja kati ya Dola za Marekani 7,000 - 12,000, na ajira zenye staha kwa angalau asilimia 50 ya Watanzania.

Na Mwandishi Wetu, Dar

Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA) imewajengea uwezo makandarasi kuhusu mazingira ya haki katika mchakato wa zabuni za umma, ili waweze kudai haki zao pindi wanapoona hawakutendewa haki kwenye michakato ya zabuni za umma walizoshiriki.

Wasilisho la PPAA limewasilishwa na Mkuu wa Sehemu ya Huduma za Sheria PPAA, Bi. Agnes Sayi ambaye alimwakilisha Katibu Mtendaji wa PPAA, Bw. James Sando katika Mkutano wa Mashauriano na Wadau wa Sekta ya Ujenzi kwa Mwaka 2026 ulioandaliwa na Bodi ya Wakandarasi (CRB) tarehe 13 – 14, Agosti, 2026 Jijini Dar es Salaam. 

Bi. Sayi amesema kuwa, ununuzi wa umma ni zaidi ya utaratibu wa kununua kazi za ujenzi, bidhaa au huduma; ni chombo cha sera ya maendeleo kinachochochea ukuaji wa uchumi, ajira, kuwezesha makandarasi wazawa kushiriki katika miradi ya Serikali na kuhakikisha matumizi bora ya fedha za umma. 

“Mazingira ya haki katika mchakato wa zabuni za umma ni mfumo unaohakikisha washiriki wote wanatendewa kwa usawa, wanashindana kwa kutumia masharti yanayofanana, na maamuzi yote yanafanywa kwa kuzingatia sheria, kanuni na masharti ya nyaraka za zabuni,” amesema Bi. Sayi

“Mazingira ya haki katika zabuni za umma ni sehemu ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050,” Bi. Sayi ameongeza.

Kadhalika, Bi. Sayi ameongeza kuwa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inahitaji mfumo wa ununuzi wa umma unaozingatia misingi ya haki, uwazi, uwajibikaji na ushindani wa haki. 

“Maamuzi ya PPAA yanaonesha kuwa mazingira ya haki si suala la kisheria pekee bali ni nyenzo ya maendeleo ya Taifa. Kupitia uchambuzi wa maamuzi ‘jurisprudence’ yake, PPAA imeendelea kujenga mfumo unaolinda haki za washiriki wa zabuni, unaoimarisha uwajibikaji wa taasisi nunuzi na unaoongeza imani ya sekta binafsi kushiriki miradi ya maendeleo,” ameongeza Bi. Sayi

Bi. Sayi amewasihi makandarasi, washauri elekezi, Taasisi nunuzi na wadau wengine kuzingatia sheria na kanuni za ununuzi wa umma ili kuiwezesha Serikali kuwa na mfumo wa ununuzi unaochochea ushindani, matumizi bora ya fedha za umma na utekelezaji wenye mafanikio wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Naye Bw. Steven Masangia Msanifu wa Majengo kutoka Kampuni ya Ebenezer Architects Ltd amesema kuwa makandarasi wamekuwa wakitekeleza mikataba, ila baadhi ya vipengele vya kwenye Masharti Maalum ya Mkataba yamekuwa yakiwabana na kupelekea baadhi yao kufilisika. 

“Makandarasi hawalipwi ongezeko la riba, jambo ambalo limekuwa likituathiri kiuchumi. Tunapaswa kulipwa ndani ya muda uliowekwa kwenye mkataba ili kutuwezesha kutekeleza mikataba kwa ufanisi,” amesema Bw. Masangia

Masangia ameitaka PPAA kuendelea kutoa elimu kwa wazabuni na makandarasi ili wasichanganye malalamiko/rufaa dhidi ya uamuzi wa ununuzi na migogoro inayotokana na utekelezaji wa mkataba baada ya mkataba kusainiwa.


Mkutano wa Mashauriano na Wadau wa Sekta ya Ujenzi, umewakutanisha wadau takribani 1,000 umeongozwa na Kaulimbiu, “Dira 2025: Fursaa na Wajibu wa Makandarasi katika ujenzi wa Miundombinu Endelevu”



Na Victor Masangu,Bagamoyo

Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo Shaibu Ndemanga amewahimiza viongozi na wananchi mbali mbali wakiwemo wadau, wanafunzi, walimu,kuhakikisha wanajenga tabia ya kushiriki kikamilifu katika michezo mbali mbali kwa lengo la kuweza kujenga afya zao ikiwa pamoja na kuondokana kabisa na changamoto ya kuwa na magonjwa yasiyoambukiza.

Hayo ameyabainisha wakati wa ufunguzi rasmi wa sherehe za maadhimisho ya miaka 20 ya Baobab tangu kuzaliwa kwake ambayo yameweza kushirikisha jumla ya washiriki zaidi ya ya elfu 1000 kutoka maeneo mbali mbali wakiwemo wadau wa michezo, wanafunzi, taasisis wezeshe pamoja na viongozi mbali mbali wa serikali.

Mkuu huyo wa Wilaya amebainisha kuwa kwa sasa jamii inapaswa kubadilika na kujikita zaidfi katika kufanya mazoezi ambayo yataweza kuwasaidia katika kujenga afya zao na kuondokana kabisa na magonjwa hivyo amewahimiza wananchi wa Wilaya ya Bagamoyo na maeneo mengine kuendelea kujitokeza kwa wingi pindi inapojitokeza michezo mbali mbali kama vile mbio za Marathon na michezo mingine.

"Niwapongeze kwa dhjati uongozi wa Baobab kw akuweza kunialika katika sherehe hizi za maadhimisho ya miaka 20 na mimi kama mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo nimewza kushiriki kikamilifu katika mbio za Marathon kwa hiyo kitu kikubwa ninachowaomba wananchi ni kuwa na tabia ya kushiriki katika michezo ili kuondokana na magonjwa mbali mbali,"amebainisha Mkuu huyo.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Taasisi za Shajar Shani Swai ambaye ndio inayoimiliki shule ya Sekondari Baobab amebainisha kwamba lengo kubwa katika Marathon hiyo ni kukusanya fedha kiasi cha zaidi ya shilingi milioni 20 kwa lengo la kuweza kuwasaidia watoto wenye ulemavu na wanaoishi katika mazingira magumu.

"Tunashukuru sisi kama taasisi tumeweza kutimiza miaka 2o tangu kuanzishwa kwake na mimi napenda kusema lengo kubwa ya kufanya marathon hii ni kukusanya zaidi ya milioni 20 ambayo itaweza kusaidia katika kusaidia watoto yatima na wale amabo wanaoishi katika mazingira magumu na tunashukuru tueweza kutimiza malengo yetu,"amebainisha mkurugenzi.

Naye Mwanzilishi wa Taasisi hiyo ya Shajar Sophia Swai amebainisha kwamba wamemua kutumia maadjimisho hayo ya miaka 20 kukusanya fedha hizo ambazo zitaweza kuwasaidia watoto ambao wanaishi katika mazingira magumu pamoja na jamii mbali mbali ambazo zinauhitaji.

Katika maadhimisho hayo ya miaka 20 ya Baobab kumefanyika mbio za kuanzia kilometa 5 hadi kilometa 10 ambapo michezo mbali mbali imefanyika ikiwemo, soka,kikapu, pete,Riadha, kuvuta kamba ambapo washindi wameweza kuzawadiwa zawadi mbali mbali ya vikombe pamoja na medani.




Na Janeth Raphael - MichuziTv 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema Tamasha la Kizimkazi limekuwa kichocheo muhimu cha maendeleo ya kiuchumi na kijamii, huku eneo hilo likizidi kufunguka kwa fursa za biashara, uwekezaji na utalii kwa wananchi wa Kusini, Zanzibar na maeneo jirani.

Akizungumza leo, Ijumaa, Agosti 14, 2026, katika kilele cha Tamasha la Kizimkazi, Rais Samia amesema tangu kuanzishwa kwake mwaka 2016, tamasha hilo limeendelea kukua na kuacha alama katika maendeleo ya eneo hilo kupitia kuongezeka kwa shughuli za kiuchumi pamoja na uboreshaji wa miundombinu na huduma mbalimbali.

Rais Samia amesema mabadiliko yanayoendelea Kizimkazi yameifanya eneo hilo kuwa sehemu yenye mazingira yanayofaa zaidi kwa wafanyabiashara na wawekezaji, akiwataka kutumia fursa zilizopo kuanzisha na kuendeleza shughuli zitakazoongeza ajira na kuchochea uchumi wa eneo hilo.

“Tunawakaribisha kuja kuwekeza, mazingira mazuri ya uwekezaji yamekwishawekwa,” amesema Rais Samia, akisisitiza umuhimu wa sekta binafsi kutumia fursa zinazotokana na maendeleo yanayoendelea kufanyika Kizimkazi.

Amesema pia Serikali inaendelea na ujenzi wa uwanja wa michezo ambao ukikamilika utakuwa miongoni mwa miundombinu itakayotumika katika michuano ya AFCON 2027. Kwa kuzingatia idadi ya wageni, wanamichezo na washiriki watakaotarajiwa kufika, Rais Samia amewataka wawekezaji kuona fursa katika sekta za malazi, chakula, usafiri, burudani na huduma nyingine zitakazohitajika.



Na Mwandishi Wetu

BENKI ya DCB Commercial Bank Plc imemtangaza Dkt. Charles Stephen Kimei kuwa Mwenyekiti mpya wa Bodi ya Wakurugenzi, akitarajiwa kutumia uzoefu wake wa zaidi ya miaka 40 katika sekta ya benki, sera za fedha, udhibiti, utafiti wa uchumi na utawala bora.

Dkt. Kimei ni miongoni mwa viongozi wenye uzoefu mkubwa katika sekta ya benki na fedha nchini Tanzania, ambapo alianza safari yake ya kitaaluma katika Benki Kuu ya Tanzania (BoT), akishika nyadhifa mbalimbali za juu ikiwamo Mkurugenzi wa Usimamizi wa Benki pamoja na Mkurugenzi wa Utafiti na Sera za Kiuchumi.

Baadaye aliteuliwa kuwa Mkurugenzi Mtendaji na Afisa Mtendaji Mkuu wa CRDB Bank Plc, nafasi aliyoitumikia katika kipindi ambacho taasisi hiyo ilifanya mabadiliko makubwa kutoka benki ya ushirika na kuwa benki ya biashara yenye ushindani mkubwa.

DCB Commercial Bank imesema uzoefu wa Dkt. Kimei katika mabadiliko ya taasisi, masoko ya fedha, usimamizi na utawala bora utakuwa muhimu katika hatua ambayo benki hiyo inaendelea kuimarisha shughuli zake na kuongeza thamani kwa wateja, wanahisa na wadau wengine.

Mbali na nafasi zake za kiutendaji, Dkt. Kimei amewahi kushika nyadhifa mbalimbali za uongozi na uwakilishi katika taasisi za ndani na nje ya sekta ya benki, zikiwamo Tanzania Bankers Association, Swissport Tanzania Plc, Economic and Social Research Foundation (ESRF), Baraza la Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Tanzania Education Authority.

Kutokana na mchango wake katika sekta ya benki na fedha, Dkt. Kimei amewahi kutunukiwa tuzo mbalimbali, ikiwamo East Africa Banker Lifetime Achievement Award mwaka 2016.

DCB Commercial Bank imesema uteuzi huo unafungua ukurasa mpya wa uongozi wa benki hiyo, ukiwa na msukumo wa kuimarisha mabadiliko, ubunifu, ukuaji endelevu na uundaji wa thamani kwa benki, wateja, wanahisa na wadau wake.

Uteuzi wa Dkt. Kimei unatarajiwa kuongeza nguvu katika uongozi wa kimkakati wa DCB, kutokana na uzoefu wake mpana katika sekta ya fedha, udhibiti wa benki na usimamizi wa taasisi.




Na Mwandishi Wetu

BAADHI ya Wananchi wa Dar es Salaam hususani watumiaji wa usafiri wa Mabasi wametetea utaratibu wa Mabasi hayo kutoa huduma maeneo mengine tofauti na Kituo cha Mabasi cha Magufuli na kuutaka Uongozi wa Mkoa kulitafakari upya suala hilo.

Awali mapema wiki hii Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Albert Chalamila alitoa muda wa wiki moja hadi Agosti 21 Mwaka huu kwa mabasi yote yanayotoa huduma tofauti na Kituo cha Mabasi cha Magufuli kuondoka katika maeneo hayo na kurejea kituoni hapo.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti tangu kutolewa kwa agizo hilo, wananchi hao hususani watumiaji wa huduma hizo za Usafiri wamesema agizo hilo la Mkuu wa Mkoa lina lengo la kuwarejesha kwenye kadhia waliyokuwa wakiipata awali.

Wamesema kulingana na  jiografia ya Jiji la Dar es Salaam ni changamoto kubwa kwa abiria kutoka maeneo mbalimbali kupata 'urahisi' wa kwenda Mbezi kwa ajili ya kusafiri hususani nyakati za usiku ambapo mara nyingi usafiri huwa shida na wakati mwingine tatizo la foleni.

" Hakuna ubishi kuwa uwepo wa huduma hizi maeneo tofauti na Mbezi (Magufuli) umetusaidia kuondoa changamoto nyingi, mbali na usumbufu unaotokana na kero za wapiga debe, suala la umbali wa kukifikia kituo hicho ilikuwa ni tatizo jingine" amesema mmoja wa wananchi aliyejitambulisha kwa jina la Seif Juma

Amesema ni vyema uongozi wa Mkoa ukalitafakari upya suala hilo hasa Kipindi hiki ambapo pia safari nyingi za Mabasi zinafanyika usiku kwa madai kwamba uwepo wa 'vituo vidogo' hivyo mitaani vinasaidia kuepusha usumbufu kwa abiria ikiwemo kuepuka kuibiwa mizigo na mali zao.

Naye mwananchi Emmanuel Yesaya, abiria aliyekuwa safarini kuelekeza Mkoa wa Katavi, amesema imekuwa nafuu sana kwa wageni kutoka Mkoani kwa uwepo wa 'vituo vidogo' hivyo mitaani kwani imekuwa ikiwaondolea usumbufu Mkubwa kutokana na ugeni wao.

Amesema kwa mgeni ambaye mara ya kwanza anashuka Mbezi hukumbana na 'adha' kubwa ikiwemo usafiri kwenda eneo alilokusudia akisisitiza kuwa uwepo wa Mabasi hayo yanayopakia na kushusha mbali na Kituo cha Magufuli umeiondoa kabisa changamoto hiyo.

Wamesema tangia kuanza kwa huduma hizo, kwa kiasi kikubwa kumesaidia abiria wengi kuondokana kero zikiwemo za kupoteza mizigo yao sambamba na kero ya usafiri kutoka maeneo watokayo kwenda Kituo Cha Magufuli huku pia wakiitumia nafasi hiyo kuishukuru Serikali kwa kuruhusu uwepo wa 'vituo hivyo miaka michache iliyopita.

Hata hivyo Uongozi wa Chama Cha Wamiliki wa Mabasi Tanzania(TABOA)  haukupatikana kulizungumzia suala hilo huku ikielezwa kuwa Utaratibu wa uwepo wa vituo hivyo mitaani ulitokana na Baraka za Serikali huku Mamlaka ya Usimamizi wa Huduma za Usafiri nchini (LATRA) ikiweka utaratibu wa utoaji wa vibali vya Mabasi kutoa huduma hizo katika maeneo hayo.



Na Janeth Raphael -MichuziTv 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amewataka Watanzania kulinda amani, usalama na utulivu wa nchi, akisisitiza kuwa misingi hiyo ndiyo nguzo kuu inayowezesha uwekezaji, ukuaji wa uchumi, utalii, biashara, ajira na maendeleo ya jamii.

Akihitimisha Tamasha la Kizimkazi Festival leo Ijumaa, Agosti 14, 2026, visiwani Zanzibar, Rais Samia amesema Tanzania imeendelea kupata mafanikio katika maeneo mbalimbali kutokana na kuwepo kwa mazingira ya amani na utulivu, hivyo wananchi wanapaswa kutambua thamani ya amani na kuilinda kwa nguvu zote.

Amesema maendeleo yanayoonekana nchini, ikiwemo kuongezeka kwa shughuli za uwekezaji, utalii, biashara na huduma za jamii, yanahitaji mazingira salama na yenye utulivu ili yaendelee kukua na kuwanufaisha wananchi. Kwa mujibu wa Rais Samia, juhudi za Serikali za kufungua fursa za kiuchumi na kijamii haziwezi kuzaa matokeo yaliyokusudiwa iwapo amani na usalama vitavurugwa.

Rais Samia amesisitiza kuwa Tanzania haiwezi kufikia malengo yake ya maendeleo endapo itaingia katika mazingira ya vurugu na machafuko, kwa kuwa hali hiyo inaweza kuvuruga shughuli za kiuchumi, kudhoofisha uwekezaji, kuathiri utalii na biashara, pamoja na kupunguza fursa za ajira zinazolengwa kuwafikia Watanzania, hususan vijana.

Kwa msisitizo, Rais Samia amewataka Watanzania kutolichukulia suala la amani kama jambo la kawaida au la kujihakikishia milele, bali kulitambua kama tunu muhimu inayohitaji kulindwa na kila mmoja. Amesema amani ndiyo mazingira yanayowezesha wananchi kufanya kazi, kufanya biashara, kuwekeza, kusoma na kushiriki katika shughuli mbalimbali za maendeleo bila hofu.

Aidha, amewataka vijana kuwa mstari wa mbele katika kulinda amani ya nchi na kutokubali kushawishiwa kufanya vitendo vinavyoweza kusababisha machafuko au kuvuruga utulivu wa taifa, akisisitiza kuwa kizazi cha sasa kina wajibu wa kuhakikisha Tanzania inaendelea kuwa nchi salama kwa ajili ya vizazi vijavyo.

“Uwekezaji, maendeleo tunayoyaona hapa; uwekezaji, utalii, biashara, ajira na huduma za jamii hayawezi kustawi katika mazingira ya vurugu na uvunjifu wa amani. Niwaombe Watanzania wenzangu hususan vijana msikubali kuharibu amani ya nchi yenu. Amani ndiyo kila kitu katika maisha yetu,” amesema Rais Samia.

Amesema kulinda amani ni zaidi ya kulinda utulivu wa nchi, kwani ni kulinda fursa za kiuchumi, ajira, uwekezaji, utalii, biashara na huduma zinazowezesha maisha ya wananchi kuendelea kuboreka. Kwa msingi huo, amewataka Watanzania wote kuendelea kushirikiana katika kuhakikisha Tanzania inabaki kuwa nchi yenye amani, usalama na utulivu ili safari ya maendeleo iendelee kwa kasi.









 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amewataka wananchi wa Kizimkazi na maeneo ya Kusini Unguja kutunza na kudumisha miradi ya maendeleo, ikiwemo maji, afya na barabara, ili iendelee kutoa huduma bora kwa wananchi.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, tarehe 14 Agosti 2026, katika kilele cha Tamasha la Kizimkazi 2026 kilichofanyika Uwanja wa Mwehe, Makunduchi, Mkoa wa Kusini Unguja.

Amesema miradi hiyo ni muhimu katika kuboresha maisha ya wananchi na kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii, hivyo wananchi wanapaswa kushirikiana na Serikali katika kuitunza na kuhakikisha inatumika kwa malengo yaliyokusudiwa.

Aidha, Rais Dkt. Mwinyi amesema Tamasha la Kizimkazi limeendelea kuwa jukwaa muhimu la kutangaza utalii, utamaduni na fursa za uwekezaji, kukuza vipaji, pamoja na kuwaunganisha wafanyabiashara na wajasiriamali na masoko mapya.

Ameipongeza Kamati ya Maandalizi kwa kuendelea kulikuza tamasha hilo na kusisitiza kuwa Serikali itaendelea kuunga mkono matukio yanayochangia kukuza utalii, utamaduni, biashara, ajira na kipato kwa wananchi.

Tamasha la Kizimkazi 2026 lilifunguliwa tarehe 12 Agosti 2026 na Rais Dkt. Mwinyi na kuhitimishwa leo, tarehe 14 Agosti 2026, na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika Uwanja wa Mwehe, Makunduchi, Mkoa wa Kusini Unguja. 














NA: MWANDISHI WETU, ZANZIBAR 

Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake wa Chama Cha Mapinduzi (UWT) Taifa, Mary Chatanda, ameungana na viongozi na wananchi katika Tamasha la Kizimkazi katika mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar.

Akizungumzia tamasha hilo,  Agosti 13, 2026, Chatanda amesema, linasaidia kukuza upendo, mshikamano na maendeleo miongoni mwa viongozi na wananchi, hivyo linapaswa kuendelezwa. 

"Tamasha la Kizimkazi linawaleta watu pamoja kutoka maeneo tofauti nchini, hili ni jambo kubwa sana, tunaongea na kubadilishana mawazo. Pia, miradi ya maendeleo kama ya elimu, afya, maji inazinduliwa katika kutatua kero za wananchi," amesema Chatanda

Aidha, amepongeza suala la utamaduni kuenziwa katika tamasha hilo, kwani utamaduni una umuhimu mkubwa katika kuliheshimisha taifa na kukuza maendeleo.

"Upekee mwingine wa tamasha hili ni kuenzi utamaduni wetu yaani mavazi, vyakula, ngoma za asili, lugha yetu ya Kiswahili, tukumbuke kuwa utamaduni unaibua fursa za kiuchumi katika kuongeza kasi ya maendeleo," amesisitiza.

Katika tamasha hilo, Chatanda ameshiriki uzinduzi na ukaguzi wa mradi wa Makaazi wa Amani (Amani Residency) na upandaji miti katika Kituo cha Afya Kizimkazi.

Viongozi mbalimbali wakiwemo Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, Dk. Hussein Mwinyi, mawaziri, wabunge, viongozi wa Chama, serikali na wananchi mbalimbali wameshiriki tamasha hilo ambalo linagusa nyanja zote za kijamii, kiuchumi na kisiasa katika kukuza maendeleo nchini.










Top News