Azindua boti mbili za kisasa kufanya doria baharini, maziwa makuu



Na Mwandishi Wetu 

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba ametoa siku 14 kwa wizara na taasisi zinazohusika na Kituo cha Kitaifa cha pamoja cha Oparesheni zipeleke wawakilishi ili kianze kufanya kazi mara moja.

"Wizara na taasisi zote zinazohusika na utekelezaji wa majukumu katika Kituo cha Kitaifa cha pamoja cha Oparesheni zipeleke wawakilishi wote wanaohitajika ndani ya siku 14 kuanzia leo. Kituo hiki kianze kazi mara moja ili kuleta tija inayokusudiwa," amesema Waziri Mkuu. 

Dkt. Mwigulu ametoa wito huo leo (Ijumaa, Julai 31, 2026) wakati akizungumza na washiriki wa hafla ya makabidhiano na uzinduzi wa boti mbili za doria aina ya PB Sailfish 02 na PB Sailfish 03 iliyofanyika bandarini, jijini Dar es Salaam. Boti hizo zimenunuliwa kwa thamani ya dola za Marekani milioni 1.6. 

Amezitaka Wizara za Muungano zinazohusika na suala hilo zishirikiane ili kuziba chochoro zote ambazo zingetumiwa na wahalifu katika eneo hili tunalolilenga na hasa katika mipaka ya mwambao wa bahari.

Ili kuhakikisha boti hizo zinafanya kazi kama inavyotarajiwa, Waziri Mkuu ameziagiza wizara na taasisi zote za umma zinazohusika katika matumizi ya boti hizi za doria zitenge fedha kwa ajili ya kazi za boti hizi.

"Ninasisitiza suala la kutenga bajeti ili kazi za doria zisikwamishwe na ukosefu wa bajeti.  Nimekuwa nikikutana na kesi kama hizo mikoani ambapo Mheshimiwa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan alinunua ambulance za kisasa na nyingine zina ICU lakini zinashindwa kuhudumia wagonjwa kwa wakati kwa kukosa mafuta. Hili linakinzana na dhamira njema ya Mheshimiwa Rais ya kutaka kuokoa maisha ya Watanzania pindi wanahitaji huduma hizo," amefafanua.

Akielezea umuhimu wa boti hizo za doria, Waziri Mkuu amesema makabidhiano ya boti hizo ni tukio muhimu kiuchumi kwa sababu zinaenda kulinda mazao yatokanayo na uchumi wa bluu. Amesema uhitaji wa boti hizo umekuwa ni kilio cha muda mrefu tangu yeye akiwa Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi.

Amesema upatikanaji wa boti hizo mbili, utaimarisha ulinzi hasa ikizingatiwa kwamba Tanzania ni lango la nchi nyingi zikiwemo za Afrika Mashariki na za SADC lakini usalama utakaokuwepo unahusu Tanzania na wananchi wa hizo nchi jirani. "Wananchi kutoka nchi hizo watakuwa na uhakika wa usalama watakapotumia lango la bandari ya Dar es Salaam," amesisitiza.

Mapema, akimkaribisha Waziri Mkuu kuzungumza na washiriki wa hafla hiyo, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Prof. Palamagamba Kabudi alisema ununuzi wa boti mbili za doria aina ya PB Sailfish 02 na PB Sailfish 03 ulifanyika baada ya kukamilika kwa taratibu zote za manunuzi ambapo mkataba wa ununuzi ulisainiwa Julai 29, 2025 kati ya Chuo cha Mipango na Maendeleo Vijijini na Kampuni ya Yamaha Motors Co. Ltd.

“Ujenzi wa boti hizo ulifanyika nchini Japan kwa kuzingatia vipimo na viwango vya kimataifa vilivyokubaliwa na wataalamu wa Serikali. Hadi kukamilika kwake, ujumbe wa wataalamu kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, TASAC, UNDP na Chuo cha Mipango ulifanya ziara za ukaguzi ili kujiridhisha na ubora wa kazi iliyotekelezwa,” alisema.

Naye, Balozi wa Japan nchini Tanzania, Mikami Yoichi alisema kijiografia Tanzania na Japan ziko mbali lakini zinaunganishwa na bahari za Hindi na Pasifiki na kwamba uwepo wa usalama kwenye mipaka ya baharini, kuwahakikishia wananchi wake usalama wa maisha yao.

Alisema ana imani kwamba Serikali ya Tanzania itahakikisha boti hizo zinatumika kwa miaka mingi kwa faida ya vizazi vijavyo.






 

Na Mashaka Mhando, Mbeya

VIWANJA vya Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU) Mkoa wa Mbeya vilitikiswa na shangwe na nderemo kufuatia mkutano mkubwa uliowakutanisha maelfu ya madereva wa bodaboda na bajaji wa Jiji hilo ana kwa ana na Mkuu wao wa Wilaya, Mhe. Solomon Itunda kuzungumzia amani na utulivu.

Mkutano huo, ambao ulitawaliwa na hali ya kirafiki na maelewano, haukuwa tu wa kutoa maagizo, bali ulikuwa ni jukwaa la kimkakati la kuwakumbusha vijana hao nafasi yao nyeti katika uchumi na usalama wa Jiji la Mbeya.

Akizungumza huku akishangiliwa na umati huo, Mhe. Itunda aliwaeleza madereva hao ukweli usiofichika kuwa wao ni injini muhimu ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi kwa mustakabali wa nchi.

Alisema kutokana na asili ya kazi yao ya kukutana na mamia ya wananchi kila siku, wana nguvu kubwa ya kujenga au kubomoa taswira ya jiji katika sekta ya usafiri kwa kuwaeleza tofauti na uhalisia wa nchi inavyoendeshwa.

Hivyo, Mkuu huyo wa Wilaya, ambaye amekuwa akisifika na wananchi wa Mbeya kama 'Mzee wa busara', aliwasihi madereva hao wa bodaboda na bajaji kuendesha vyombo vyao kwa umakini mkubwa na kuzingatia sheria za usalama barabarani ili kunusuru maisha yao na ya abiria wao.

"Ndugu zangu wa bodaboda na bajaji, sisi ni watu wa Mbeya, tunapokuwa kazini tulinde amani yetu. Nyie mkiwa mabalozi, lakini pia ni vizuri mkalinda amani ya nchi kwa kuhubiri amani kwa abiria wenu," alisema Itunda.

Katika kile kilichoonyesha kutambua mazingira wezeshi ya biashara, Mkuu huyo wa Wilaya alitumia jukwaa hilo kumpongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan. Mhe. Itunda aliweka wazi kuwa msingi imara wa amani, utulivu, na uhuru wa kiuchumi uliojengwa na Rais Samia ndio unaowapa vijana wengi fursa ya kujitafutia kipato mitaani bila bughudha.

Akifafanua kuhusu fursa za kiuchumi, DC Itunda aliwafafanulia wananchi hao kuwa awali mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na Halmashauri ya Jiji haikuwa ikiwafikia walengwa, lakini Rais Samia ameweka utaratibu mpya unaohakikisha kila kijana aliyekuwa kwenye kikundi ananufaika.

Aliwataka vijana hao, kama miongoni mwa wanufaika, kulinda fedha za mikopo wanayopewa na kuirejesha kwa wakati, ili asilimia hiyo 10 iweze kuwanufaisha vijana wengi zaidi wa Jiji hilo baada ya maboresho hayo makubwa.

DC Itunda aliwataka bodaboda hao kuunga mkono juhudi hizo za Rais kwa vitendo, huku wakiweka maslahi ya Tanzania mbele, ili kuhakikisha makundi ya vijana, wanawake, na watu wenye ulemavu yanawezeshwa na kuifanya Tanzania yenye watu milioni 65 kupiga hatua kiuchumi.

Hata hivyo, kama Mwenyekiti wa Kamati ya Usalama ya Wilaya, Mhe. Itunda hakusita kugusa mshipa wa usalama. Aliwapa onyo na kuwasihi vijana hao kutokubali kutumika kama daraja la uhalifu. Aliwaomba wawe walinzi wa kwanza wa Jiji kwa kutoa taarifa za siri kwa vyombo vya dola mara wanapobaini watu wasioeleweka.

"Jiepusheni na makundi yenye mwelekeo wa kuvunja sheria. Ushirikiano wenu na Serikali ndiyo nguzo pekee itakayotuhakikishia Mbeya inabaki kuwa salama kwa maendeleo endelevu," alisisitiza Mhe. Itunda.

Kauli hizo za DC ziliingia vizuri masikioni mwa madereva hao, ambao kwa upande wao hawakuwa na hiyana. Wakizungumza kwa niaba ya wenzao, viongozi wa bodaboda waliipongeza Serikali kwa kuendelea kuwathamini na kutatua changamoto zao.

Kama ishara ya kukubaliana na mwongozo wa DC Itunda, madereva hao waliweka ahadi nzito mbele ya mamlaka kuwa kuanzia sasa watakuwa mabalozi wazuri wa usalama barabarani, watafichua wahalifu wote wanaochafua taswira ya kazi yao, na watalinda amani ya Mbeya kwa nguvu zao zote.








Na Mwandishi wetu, Mirerani

WADAU wa madini ya Tanzanite, mji mdogo wa Mirerani wilayani Simanjiro, Mkoani Manyara, wamechangia Sh23.6 milioni kwa ajili ya kuboresha huduma za afya na kuokoa maisha ya watoto wachanga njiti.

Lengo ni kuunga mkono mkoa wa Manyara, ambao umeandaa mbio za hisani za kuchangia ujenzi wa jengo la mama na mtoto na kuboresha huduma za afya zitakazofanyika mjini Babati, Agosti 22, 2026 mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Waziri Mkuu Mwigulu Nchemba.

Wadau hao wa madini ya Tanzanite, wamechangia kiasi hicho mbele ya Mkuu wa mkoa wa Manyara Queen Cuthbert Sendiga kwa nia ya kukusanya kiasi cha Sh1.6 bilioni cha kuanza ujenzi kwenye hospitali ya wilaya ya Hanang'.

Sendiga amewashukuru wadau hao wa madini ya Tanzanite kwa kuchangia fedha hizo ili kufanikisha ujenzi huo wa wodi ya watoto njiti.

"Mmefanya jambo kubwa mno kwani watoto njiti 3,000 kila mwaka kwenye mkoa wetu huwa wanazaliwa kwa hiyo tunataka tufanye jambo la baraka kwa watoto wanaozaliwa chini ya miezi tisa," amesema RC Sendiga.

Mkuu wa wilaya ya Simanjiro, Fakii Lulandala ameeleza kwamba wadau wa madini ya Tanzanite watajitokeza kwa wingi kuunga mkono mbio hizo za kusaidia watoto njiti.

"Mimi binafsi nitakimbia kilomita tano na wana Simanjiro kwa umoja wetu tutashiriki  kwa wingi mbio hizo kuchangia matibabu ya watoto wetu," amesema Lulandala.

Mkurugenzi wa JS Magezi, William Magezi wanaochimba kitalu D extension kwa kushirikiana na Tanzanite Afrika, amesema wadau wanaochangia wanakuwa wanatoa sadaka ambayo pia inakuwa toba kwa makosa yaliyofanyika.

"Mkurugenzi mwenza wa Tanzanite Africa Will Mushi alichangia Sh2 milioni na mimi nachangia Sh2 milioni hivyo jumla tumetoa Sh4 milioni," amesema Magezi.

Mkurugenzi wa JN Mining Justin Nyari ambaye amechangia Sh2 milioni ameeleza kuwa wadau wa nyanja tofauti washirikishwe katika sadaka hiyo.

"Hili jambo ni zuri mno katika kuokoa maisha ya watoto wetu, ushauri wangu wote wapitiwe kwa kupitia viongozi wetu wa kata na vitongoji ili kila mmoja ashiriki vile alivyojaliwa," amesema Nyari.

Mwenyekiti wa chama cha wafanyabiashara wa madini mkoa wa Manyara, Mokia Ole Mrefu amesema ili kuunga mkono tukio hilo, jumanne ijayo watafanya kikao na wafanyabiashara wa madini ya Tanzanite ili kwa umoja wao nao wachangie.

"Pia nikiwa hapa hapa mdau wa maendeleo wa mkoa wa Manyara,  Taiko Ole Kulunju, amechangia kwa kutuma Sh1 milioni na mimi binafsi nachangia Sh500,000 ili kumuunga mkono RC wetu Sendiga," amesema Ole Mrefu.

Mmiliki mwingine wa mgodi wa madini ya Tanzanite, Joseph Manga ambaye amechangia Sh1 milioni ametoa ombi la kurekebishwa changamoto ya bei ya kibali cha kununua zana za milipuko.

"Tunakuunga mkono RC wetu kwenye hili ila tunakuomba utuangalie suala la sisi wachimbaji kulipia Sh100,000 kwa kila kibali cha kununua milipuko siyo sawa, kibali kiwe kimoja kwa bei hiyo hiyo," amesema Manga.



MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA) imefanya kikao na wadau wa michezo ya kubahatisha ikiwemo waendeshaji kutoka makampuni mbalimbali kwa lengo la kujadili masuala ya kodi.

Akimuwakilisha Kamishna wa Kodi za Ndani katika kikao hicho kilichofanyika leo tarehe 31 Julai, 2026 Serena Hotel jijini Dar es Salaam, Naibu Kamishna wa Walipakodi wa Kati Godwin Barongo amesema kuwa kodi itokanayo na michezo ya kubahatisha imeendelea kuwa na manufaa makubwa kwa Tanzania.

Barongo ameeleza kuwa kwa kipindi cha miaka tisa ya fedha kuanzia 2017/2018 ambapo kodi katika michezo hiyo ilianza kukusanywa hadi 2025/2026, mchango wa sekta hiyo umefikia takriban Shilingi Trilioni 1.463.

“Mchango huu mkubwa unaonesha umuhimu wa sekta hii katika kuchangia maendeleo ya taifa, na nawapongeza sana waendeshaji na wadau wote kwa ushirikiano mnaoendelea kuutoa,” amesema Barongo.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Oparesheni za Kimkakati wa Bodi ya Michezo ya Kubahatisha Tanzania Kabora Mboya ameipongeza TRA kwa kuendelea kuwakutanisha wadau wa sekta hiyo huku akisisitiza umuhimu wa ushirikiano endelevu katika kupata mafanikio.

Nao wadau wa sekta hiyo wamesema wapo tayari kuendelea kulipa kodi na kuiomba TRA na taasisi zingine za serikali kuendeleza utaratibu wa kukutana na wadau hao ili waweze kuimarisha ushirikiano na ufanisi wa utekelezaji wa wajibu wao.




📌 Shule ya Sekondari Nkololo yaachana na kuni pamoja na mkaa

Bariadi, Simiyu📍

Timu ya Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa imezindua rasmi mradi mkubwa wa ujenzi wa miundombinu ya nishati safi ya kupikia katika Shule ya Sekondari Nkololo, iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Bariadi Vijijini mkoani Simiyu.

Mradi huo, uliozinduliwa tarehe 30 Julai 2026, una lengo la kutokomeza kabisa matumizi ya kuni na mkaa katika taasisi zinazohudumia zaidi ya watu 100 kwa siku, kama sehemu ya kulinda mazingira na afya za Watu.

Akizungumza mara baada ya kukagua na kuzindua mradi huo, Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa, Bw. Wazo Michael Mwang’onda, aliipongeza Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kwa utekelezaji madhubuti wa mkakati huo wa serikali.

Bw. Mwang’onda alibainisha kuwa mradi huo utaleta tija kubwa kwa shule hiyo yenye jumla ya wanafunzi 606.

“Kupitia mradi huu, Serikali itapunguza kwa kiasi kikubwa matumizi ya kuni na mkaa wa kawaida. Hali hii itaboresha afya na usalama wa wanafunzi, walimu, pamoja na wapishi wanaotumia jiko hili kila siku,” alisema Kiongozi huyo.

Kwa upande wake, Mhandisi wa Miradi ya Nishati kutoka REA, Mha. Davidi Malima, alifafanua kuwa wakala huo umewekeza shilingi milioni 15 katika Shule ya Sekondari Nkololo. Fedha hizo zimefanikisha ununuzi wa majiko mawili makubwa yenye uwezo wa lita 200 kila mmoja, pamoja na usimamishaji wa tanki la gesi ya kupikia (LPG) lenye ukubwa wa tani moja.

Mha. Malima aliongeza kuwa mradi huo ni sehemu ya mpango mkubwa wa kitaifa unaolenga kuzifikia taasisi 453 katika mikoa yote nchini, ambapo jumla ya shilingi bilioni 25.8 zimetengwa.Mpango huu ni sehemu ya utekelezaji wa Mkakati wa Taifa wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia (2024–2034) wenye lengo la kuhakikisha asilimia 80 ya Watanzania wanatumia nishati safi ifikapo mwaka 2034.

Katika kufanikisha azma hiyo, kampuni ya Taifa Gas Limited ilishinda zabuni ya kusambaza na kufunga mifumo ya gesi ya LPG kwenye taasisi, huku kampuni ya Hanny G Investment ikikabidhiwa dhamana ya kusambaza majiko banifu na masufuria makubwa kote nchini.

Utekelezaji wa mradi huu unakuja wakati ambapo takwimu za mazingira nchini zikionyesha hali ya isiyoridhisha; ambapo Tanzania inapoteza zaidi ya hekta 370,000 hadi 470,000 za misitu kila mwaka. Sehemu kubwa ya uharibifu huu inasababishwa na uvunaji wa kuni na mkaa kwa ajili ya kupikia, huku zaidi ya asilimia 90 ya kaya na taasisi nchini zikiwa bado zinategemea nishati hiyo (Kuni na mkaa wa kawaida).

Mbali na uharibifu wa mazingira, matumizi ya kuni kwenye majiko yasiyo rasmi yanasababisha uchafuzi mkubwa wa hewa ndani ya nyumba na taasisi. Moshi wa kuni unaozalisha gesi hatari za ukaa (Carbon Monoxide) na chembechembe za moshi hubeba athari kubwa za kiafya, ikiwemo magonjwa ya mfumo wa upumuaji, matatizo ya macho, na hata vifo vya mapema kwa Watumiaji wa nishati hiyo.







Taasisi za NMB Foundation na Mercy Corps Tanzania zimesaini makubaliano ya utekelezaji wa mradi wa Evolve wenye thamani ya Shilingi bilioni 2.6 utakaotekelezwa kwa miaka miwili ili kukuza biashara zinazohusiana na usafiri wa vyombo vya moto vinavyotumia umeme jijini Dar es Salaam.

Mradi huo unaofadhiliwa na Umoja wa Ulaya kupitia Enabel unalenga kuwawezesha wanawake, vijana na wafanyabiashara wa E-Mobility kupitia mafunzo ya biashara, ushauri wa kitaalamu pamoja na upatikanaji wa ruzuku na mikopo.

Meneja Mkuu wa NMB Foundation, Nelson Karumuna, alisema awamu ya kwanza itanufaisha zaidi ya biashara 25 huku Mercy Corps ikiongoza utekelezaji wa shughuli mbalimbali za kuwawezesha wabunifu na wafanyabiashara waliopo katika sekta hiyo.

Washirika wa mradi wanaamini ushirikiano huo utachangia ukuaji wa sekta ya E-Mobility, kuongeza ajira na kuharakisha matumizi ya teknolojia za usafiri safi nchini sambamba na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Meneja Mkuu wa NMB Foundation, Nelson Karumuna (katikati), na Mratibu wa Mercy Corps Tanzania, Anthony Salota, wakionyesha makubaliano ya utekelezaji wa Mradi wa Evolve mara baada ya kusaini MoU jijini Dar es Salaam. Kushoto ni Virginie Hallet, Mkurugenzi Mkazi wa Enabel Tanzania, na kulia ni Marc Stalmans, Mkuu wa Ushirikiano wa Umoja wa Ulaya (EU) nchini Tanzania.

eneja Mkuu wa NMB Foundation, Nelson Karumuna, akipeana mkono na Mratibu wa Mercy Corps Tanzania, Anthony Salota, baada ya kusaini Makubaliano ya Utekelezaji wa Mradi wa Evolve. Kushoto ni Virginie Hallet, Mkurugenzi Mkazi wa Enabel Tanzania, na kulia ni Marc Stalmans, Mkuu wa Ushirikiano wa Umoja wa Ulaya nchini Tanzania.










Na Victor  Masangu,Bagamoyo 

Mwenyekiti wa Jumuiya ya  ya Wazazi Taifa Ndg. Fadhili Maganya amekemea vikali baadhi  viongozi wa CCM  wakiwemo madiwani na wabunge kuachana na vitendo vya kupanga safu hasa katika kuelekea kwenye uchaguzi wa mwaka 2027.

Hayo ameyabainisha  wakati wa ziara yake ya kikazi yenye lengo la kuweza kukiimarisha chama pamoja na jumuiya zake zote ikiwa samba samba na kuangalia uhai wa chama.

"Kitu kikubwa ninachowaomba viongozi,madiwani pamoja na wabunge  kuondokana kabisa na masuala ya kuamua kupanga safu kabla ya uchaguzi lkn kitu kikubwa wanaotaka kugombea ruksa kugombea nafasi mbali mbali,"amesema Mwenyekiti huyo.

Pia amefafanua kwamba mwakani ni kipindi cha uchaguzi hivyo hakusita kuwaasa wanachama wote kuanzia ngazi za mashina wasisite kujitokeza katika kugombea nafasi mbali mbali.

Kadhalika ameupongeza uongozi wa Wilaya ya Kisarawe kwa kuweza kusimamia vizuri utekelezaji wa ilani na ukusanyaji wa fedha za mapato ya ndani ambazo zimekwenda kutekeleza miradi ya maendeleo.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe Petro Magoti amesema kuwa hali ya  mwenendo  katika utekelezaji wa  miradi ya maendeleo inakwenda vizuri.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Mkuranga Nasri Ally amebainisha kuwa wameweza kufanikisha kukusanya mapato ya ndani kwa asilimi 113 na kuongeza  wana miradi 9 ya kimkakati ikiwemo mradi wa ujenzi wa ya kisasa.

Naye Mwenyekiti wa chama cha mapinduzi (CCM) Wilaya ya Kisarawe Halfan Sika amebainisha kwamba  wameweza kutekeleza ilani ya chama kwa vitendo ikiwa sambamba na kushirikiana na serikali katika miradi mbali mbali.

Mbunge wa Jimbo la Bagamoyo Kisarawe Selemani Jafo amempongeza Mwenyekiti wa  Taifa kwa kufanya ziara hiyo ya kikazi ambayo itaweza kuleta tija katika maendekeo kwa wananchi.

Mwenyekiti wa wazazi Mkoa wa Pwani Jackson  KItuka amewahimiza viongozi kuhakikisha wanapambana na winbi la baadhi ya matapeli wa ardhi kwani wamekuwa wakisababisha migogoro  ya ardhi. 

Akiwa Wilayani Mkuranga ameridhishwa na uchapa kazi wa Mkuu wa Wilaya ya Mkuranga kwa kuweza kusimamia vema utekelezaji wa miradi mbali mbali.

Mwenyekiti wa Jumuiya ya wazazi ya CCM Taifa ameendelea na ziara yake ya kikazi  katika Wilaya za Kisarawe pamoja na Wilaya ya mkuranga ambapo ametembelea miradi ya maendeleo ukiwemo Hospitali ya Kisarawe,daraja la Kisopwa,shule ya msingi sanze na chuo cha Veta mkuranga.






Na Janeth Raphael - MichuziTv

Benki ya Ushirika Tanzania (COOP Bank Tanzania) imefanya Mkutano Mkuu wake wa Pili tangu kuanzishwa kwake, ambapo viongozi na wanahisa walipokea taarifa ya mafanikio makubwa ya utendaji wa benki hiyo katika kipindi cha miaka miwili, yakionyesha ukuaji wa kasi katika sekta ya benki nchini.

Akizungumza wakati wa mkutano huo, Mkurugenzi Mtendaji wa COOP Bank Tanzania, Godfrey Ng'urah, amesema mkutano huo umekuwa fursa ya kutafakari safari ya mageuzi ya benki hiyo na hatua mbalimbali zilizofikiwa tangu kuanzishwa kwake.

Amesema mafanikio hayo yametokana na uongozi uliojikita katika mabadiliko, ambao umewezesha benki kuongeza kwa kiwango kikubwa rasilimali, wafanyakazi, matawi pamoja na ukubwa wa mizania ya benki ndani ya muda mfupi.

Ng'urah amesema viashiria vya utendaji vinaonesha kuwa COOP Bank ndiyo benki inayokua kwa kasi zaidi nchini kwa sasa, huku ikishuhudia ongezeko kubwa la wafanyakazi, upanuzi wa mtandao wa matawi na kuimarika kwa huduma zinazowafikia wateja katika maeneo mbalimbali.

Kwa upande wa utoaji wa mikopo, alisema benki imeendelea kuwawezesha wanachama wa vyama vya ushirika, wakulima, wafanyakazi, wafanyabiashara pamoja na taasisi mbalimbali za ushirika, ambapo kitabu cha mikopo kimeongezeka kutoka Sh bilioni 14 mwaka 2024 hadi kufikia Sh bilioni 102 mwaka 2025.

Aidha, amesema amana za wateja zimeongezeka kutoka Sh bilioni 15 hadi kufikia Sh bilioni 114 mwishoni mwa mwaka wa fedha uliopita, huku mtaji wa wanahisa ukikua kutoka Sh bilioni 27 hadi Sh bilioni 42, jambo linaloonyesha kuimarika kwa msingi wa kifedha wa benki hiyo.

Mkurugenzi huyo amebainisha kuwa COOP Bank imeendelea kupanua wigo wa bidhaa na huduma zake bunifu kwa kuanzisha akaunti nafuu zinazorahisisha uwekaji wa amana pamoja na kuwekeza katika miundombinu ya kidijitali inayowawezesha wateja kupata huduma kwa urahisi zaidi.

Ameongeza kuwa benki hiyo imezindua huduma ya COOP PESA, mfumo wa kisasa wa huduma za kibenki kupitia simu za mkononi unaowawezesha wateja kufanya miamala mbalimbali kwa urahisi, usalama na wakati wowote bila kulazimika kufika tawi.

Ng'urah amesema COOP Bank itaendelea kuwekeza katika ubunifu wa huduma za kifedha na teknolojia ili kuongeza ujumuishi wa kifedha, kuwafikia Watanzania wengi zaidi na kuchochea maendeleo ya sekta ya ushirika pamoja na uchumi wa nchi kwa ujumla.



Na Said Mwishehe,Michuzi TV

SERIKALI imeanzisha Chama cha Wahandisi wa Nishati (Association of Energy Engineers - AEE) Tanzania Chapter, hatua inayolenga kuimarisha ufanisi wa matumizi ya nishati, kupunguza upotevu wa umeme na kusaidia ukuaji endelevu wa sekta ya viwanda.

Chama hicho kilichoanzishwa kwa ushirikiano kati ya Serikali na Shirika la Umoja wa Mataifa la Maendeleo (UNDP), kitaongoza juhudi za kukabiliana na upotevu wa nishati unaokadiriwa kufikia asilimia 10 hadi 15, huku kikihamasisha matumizi bora ya nishati katika viwanda, taasisi na majengo ya biashara.

Akizungumza wakati wa uzinduzi jijini Dar es Salaam leo Julai 31,2026, Mkuu wa Kitengo cha Usimamizi wa Mazingira wa Wizara ya Nishati, Emilian Nyanda, alisema Tanzania imeweka sera na mikakati mbalimbali ya kuboresha ufanisi wa matumizi ya nishati, lakini mafanikio yake yanategemea uwepo wa wataalamu wenye ujuzi.

“Bila kuwa na wataalamu wa kutosha, itakuwa vigumu kufikia malengo ya taifa ya kuongeza ufanisi wa matumizi ya nishati,” alisema Nyanda.

Alisema utekelezaji wa Mpango Kazi wa Ufanisi wa Nishati umewezesha kuzalishwa kwa wakaguzi wa nishati 60 wenye ithibati, watakaosaidia kufuatilia matumizi ya nishati na kubaini maeneo yanayohitaji maboresho.

Nyanda alisema wataalamu hao watafanya ukaguzi katika viwanda, majengo ya biashara na taasisi za umma ili kubaini njia za kupunguza matumizi ya nishati bila kuathiri uzalishaji au utoaji wa huduma.

Alisema matumizi bora ya nishati yatasaidia kupunguza gharama za uzalishaji, hasa katika viwanda ambako umeme ni sehemu kubwa ya gharama za uendeshaji, hivyo kuongeza ushindani wa bidhaa zinazozalishwa nchini.

Aliongeza kuwa chama hicho kitatoa ushauri wa kitaalamu kwa Serikali kuhusu sera na mikakati ya nishati, huku kikihamasisha matumizi yenye uwajibikaji na kupunguza upotevu usio wa lazima.

Nyanda alisema kupunguza upotevu wa nishati kutapunguza pia shinikizo la uwekezaji katika miradi mipya ya umeme kwa kuhakikisha nishati inayozalishwa, ikiwemo kutoka Mradi wa Kufua Umeme wa Julius Nyerere, inatumika kwa ufanisi.

Meneja wa Maendeleo ya Vipaji wa UNDP, Veronica Sigalla, alisema AEE Tanzania Chapter inapaswa kuwa jumuishi kwa kutoa fursa kwa vijana, wanawake, wahandisi, mafundi, watafiti na wataalamu wa sekta ya nishati.

Alisema UNDP itaendelea kushirikiana na Wizara ya Nishati, Umoja wa Ulaya, Ubalozi wa Ireland na wadau wengine kuimarisha mfumo wa ufanisi wa matumizi ya nishati nchini.

Rais wa AEE Tanzania Chapter, Atupele Kilindu, alisema chama hicho kitakuwa jukwaa la wataalamu wa nishati kuimarisha ujuzi, kubadilishana maarifa, kukuza ubunifu na kuchangia utekelezaji wa malengo ya taifa katika sekta ya nishati.

“Kuanzishwa kwa AEE Tanzania Chapter kunaipa Tanzania jukwaa la kitaaluma litakalowawezesha wataalamu kuendelea kujifunza, kuendeleza ubunifu na kuunga mkono ajenda ya maendeleo endelevu ya nchi,” alisema Kilindu.

Alisema chama hicho kitaweka mkazo katika mafunzo ya kitaaluma, programu za uthibitishaji, utafiti, ubunifu, kulea wataalamu vijana na kuimarisha ushirikiano kati ya Serikali, taasisi za elimu, sekta binafsi na washirika wa maendeleo.
Mkuu wa Kitengo cha Usimamizi wa Mazingira wa Wizara ya Nishati, Emilian Nyanda (wapili kushoto) akizindua tawi la kwanza la Chama cha Wahandisi wa Nishati (Association of Energy Engineers - AEE) nchini, katika hafla iliyofanyoika leo jijini Dar es Salaam, watatu kulia ni Meneja wa Maendeleo ya Vipaji wa UNDP, Veronica Sigalla, na Rais wa AEE, Tupele Kilindu, katikati.






Na. Mtemi Sona

Dodoma. Mwenyekiti wa Ujenzi Sports Club, Arch. Ibrahim Chatila, amesema uongozi mpya umejipanga kuijenga timu hiyo kuwa ya kisasa, imara na yenye ushindani mkubwa katika mashindano yote itakayoshiriki.

Akizungumza kuhusu mikakati ya kuiboresha klabu hiyo iliyo chini ya Wizara ya Ujenzi, Chatila amesema lengo kuu ni kuunda kikosi chenye ubora wa hali ya juu kitakachokuwa na uwezo wa kushindana na timu mbalimbali nchini.

Amesema hatua za awali zitahusisha usajili wa wachezaji bora pamoja na kuimarisha benchi la ufundi kwa kuwashirikisha makocha wenye uwezo na sifa zinazohitajika ili kuongeza ushindani wa timu.

"Tunataka kuunda timu yenye wachezaji watakaoweza kuleta ushindi na ambao watazingatia weledi, nidhamu na taaluma katika kila mashindano tutakayoshiriki," amesema Chatila.

Mwenyekiti huyo ameongeza kuwa uongozi mpya uliochaguliwa umeazimia kuijenga upya Ujenzi Sports Club kwa misingi ya umoja, utawala bora na uwajibikaji kuanzia kwa viongozi, benchi la ufundi, wachezaji hadi wanachama.

Kwa mujibu wa Chatila, mafanikio ya timu hayatategemea ubora wa kikosi pekee, bali pia uimara wa mifumo ya uendeshaji wa klabu.

Mbali na masuala ya kiufundi, amesema uongozi wake umeweka mkazo katika kuimarisha uchumi wa klabu kwa kutafuta wadhamini na wadau mbalimbali watakaosaidia kuiendesha timu kwa kiwango cha kisasa.

"Lengo letu ni kuwa na klabu inayojitegemea kiuchumi, yenye uwezo wa kujiendesha na kushiriki mashindano kwa ushindani mkubwa," amesema.

Arch. Ibrahim Chatila ni Mbunifu Majengo kutoka Wakala wa Majengo Tanzania (TBA), ambayo ni moja ya taasisi zinazounda Ujenzi Sports Club. Pia ni kocha mwenye leseni ya CAF na amewahi kuwa mjumbe wa Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Singida kwa kipindi cha miaka minne.

Yeye ni miongoni mwa viongozi wapya waliochaguliwa hivi karibuni kuiongoza Ujenzi Sports Club, klabu inayoundwa na taasisi 10 zilizo chini ya Wizara ya Ujenzi.

Klabu hiyo hushiriki michezo mbalimbali ikiwemo mpira wa miguu, netiboli, riadha, kuvuta kamba na michezo mingine ya ushindani.


Top News