Bodi ya Wakurugenzi ya Shirika la Uvuvi Tanzania (TAFICO), imefanya ziara ya ukaguzi katika mradi wa Bandari ya Uvuvi Kilwa Masoko, kwa lengo la kujionea hatua ya utekelezaji wa mradi, kukagua miundombinu na maandalizi yaliyofanyika kuelekea kuanza kwa matumizi ya bandari hiyo, pamoja na kutathmini fursa zitakazotokana na uwekezaji huo katika shughuli za uvuvi na uchumi wa buluu.

Ziara hiyo imefanyika leo tarehe 20 Agosti 2026, ikiongozwa na Mwenyekiti wa Bodi hiyo Prof. Yunus D. Mgaya, ambapo Bodi hiyo imepata fursa ya kukagua maeneo mbalimbali ya bandari na kupata maelezo kuhusu hatua iliyofikiwa katika maandalizi ya kuanza kwa shughuli zake.

Akizungumza baada ya ziara hiyo, Prof. Mgaya, amesema ameridhishwa na maendeleo ya mradi huo, akieleza kuwa kukamilika na kuanza kufanya kazi kwa Bandari ya Uvuvi Kilwa Masoko kutakuwa hatua muhimu katika kuimarisha sekta ya uvuvi nchini.

"Bandari hii ina nafasi kubwa katika kuongeza ufanisi wa shughuli za uvuvi, kuongeza thamani ya mazao ya uvuvi, pamoja na kutoa fursa za ajira na biashara. Nawahimize wawekezaji kutoka ndani na nje ya nchi kutumia fursa zilizopo katika Bandari ya Uvuvi Kilwa Masoko kwa kuwekeza katika shughuli mbalimbali zinazohusiana na sekta ya uvuvi," aliongeza Prof. Mgaya

Kwa upande wake, Afisa Mtendaji Mkuu wa TAFICO, Dkt. Suleiman Kiula, ndc , amesema Shirika hilo linaendelea na mchakato wa kushirikisha sekta binafsi pamoja na wadau mbalimbali kuhakikisha bandari hiyo inaendeshwa kwa ufanisi, kwa kutoa huduma wezeshi kwa viwango bora na nafuu ili kuvutia Meli nyingi kutumia bandari hiyo ili kufikia malengo yaliyokusudiwa.

Dkt. Kiula amesema TAFICO inaendelea kutekeleza mikakati ya kushiriki kikamilifu katika kuendeleza shughuli za uvuvi wa kisasa na ukuzaji viumbe maji, ikiwemo uwekezaji katika Meli za uvuvi wa bahari kuu, uanzishaji wa mashamba ya kufuga samaki, miundombinu wezeshi, pamoja na kuongeza thamani ya mazao ya uvuvi.

"Kuanza kwa shughuli za Bandari ya Uvuvi Kilwa Masoko kutafungua fursa mbalimbali kwa wavuvi, wafanyabiashara na wawekezaji, huku kukiwa na matarajio ya kuongeza ajira na kuchochea shughuli za kiuchumi katika Wilaya ya Kilwa na maeneo mengine nchini," alieleza Dkt. Kiula.

Bandari ya Uvuvi Kilwa Masoko ni mradi wa kimkakati unaolenga kuimarisha shughuli za uvuvi nchini. Miundombinu ya bandari hiyo inajumuisha gati lenye urefu wa mita 315 la kuhudumia meli za uvuvi zaidi ya kumi kwa wakati mmoja, eneo la kuhifadhi samaki, mtambo wa kizalisha barafu na eneo la matengenezo ya meli, hatua inayolenga kuongeza ufanisi katika shughuli za uvuvi na mnyororo wa thamani wa mazao ya uvuvi.




























Na Janeth Raphael – MichuziTv 

Mfumo wa Kielektroniki wa Ununuzi wa Umma (NeST) umeendelea kuimarishwa kwa kuunganishwa na zaidi ya mifumo 30 ya taasisi mbalimbali, hatua inayolenga kurahisisha mchakato wa zabuni za umma, kuongeza ufanisi na kuimarisha uhakiki wa taarifa za wazabuni.

Hatua hiyo pia imeongeza uwezo wa Serikali kudhibiti matumizi ya nyaraka zisizo halali katika mchakato wa ununuzi wa umma, huku wazabuni wakipata unafuu wa kuwasilisha taarifa na nyaraka zinazohitajika wakati wa kushiriki zabuni.

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA), Dennis Simba, amesema maboresho hayo yanaendana na maelekezo ya Rais Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha mifumo ya Serikali inaunganishwa na kusomana ili kuwezesha kubadilishana taarifa kwa ufanisi.

Simba ameyasema hayo leo, Agosti 20, 2026, jijini Dodoma wakati akieleza utekelezaji wa bajeti ya PPRA kwa mwaka wa fedha 2025/2026 pamoja na mwelekeo wa utekelezaji wa bajeti kwa mwaka 2026/2027.

Kwa mujibu wa Simba, NeST kwa sasa imeunganishwa na mifumo zaidi ya 30 inayohusisha maeneo mbalimbali muhimu katika uthibitishaji wa taarifa za wazabuni. Mifumo hiyo inajumuisha mifumo ya kibenki na malipo, hifadhi za jamii, bodi za usajili wa wataalamu pamoja na mifumo inayohusiana na utoaji wa leseni.

Amesema kuunganishwa kwa mifumo hiyo kumeboresha kwa kiasi kikubwa namna taarifa za wazabuni zinavyothibitishwa, kwani taarifa muhimu zinaweza kupatikana na kuhakikiwa moja kwa moja kupitia mifumo husika.

Simba amesema hatua hiyo pia imepunguza uwezekano wa kuwasilishwa kwa nyaraka za kughushi katika mfumo wa NeST, kwa kuwa taarifa na nyaraka mbalimbali zinaweza kufanyiwa uhakiki kupitia mifumo iliyounganishwa.

Aidha, amesema mfumo huo umeendelea kupunguza mzigo kwa wazabuni ambao hapo awali walilazimika kuandaa na kuwasilisha rundo la nyaraka katika hatua mbalimbali za mchakato wa zabuni.

“Ndiyo maana tunasema ununuzi wa umma sasa umerahisishwa na unaweza kutumia muda mchache kwa sababu rundo la nyaraka tayari lipo ndani ya mfumo,” amesema Simba.

Amesema matumizi ya teknolojia katika ununuzi wa umma siyo tu yanalenga kurahisisha taratibu, bali pia kuongeza uwazi, ufanisi na uaminifu katika mchakato mzima wa zabuni.

Kwa hatua hiyo, NeST imeendelea kuwa nyenzo muhimu katika utekelezaji wa ununuzi wa umma kwa njia ya kielektroniki, huku kuunganishwa kwake na mifumo mingine ya Serikali na taasisi mbalimbali kukitarajiwa kuongeza zaidi ufanisi wa huduma na kuimarisha udhibiti wa taarifa katika sekta ya ununuzi wa umma.



 

Na.Mwandishi Wetu- Dodoma

KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo imeipongeza Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) kwa utekelezaji mzuri wa majukumu yake na kuitaka kuharakisha matumizi ya Mfumo wa Stakabadhi za Ghala (WRS) katika zao la parachichi ili kuongeza tija kwa wakulima.

Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Deodatus Mwanyika, ametoa pongezi hizo leo Agosti 20, 2026 jijini Dodoma baada ya Kamati hiyo kupokea na kujadili taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya WRRB kwa mwaka 2025/26.

Mhe. Mwanyika amesema Kamati imeridhishwa na utendaji kazi wa WRRB, hasa katika kushughulikia changamoto za wananchi, na kuitaka Bodi hiyo iongeze kasi katika utoaji elimu ili kuchochea matumizi ya mfumo huo katika maeneo mengine.

Akitoa ufafanuzi wa hoja za wajumbe, Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga, ameahidi kufanyia kazi maelekezo ya Kamati hiyo na kuihakikishia kuwa ataendelea kulinda majukumu ya taasisi zilizo chini yake kwa mujibu wa sheria.

Awali, akiwasilisha taarifa kwa Kamati hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa WRRB, Bw. Asangye Bangu, amesema kwa mwaka 2025/26, WRRB imetoa leseni kwa waendesha ghala 235, kusajili ghala 951, wanunuzi 390, waweka mali 2,667 na kutoa stakabadhi za ghala 214,170.


Na Munir Shemweta,Tanga

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Dkt. Leonard Akwilapo, amefanya ziara katika maeneo yenye migogoro ya ardhi katika Halmashauri ya Jiji la Tanga na Halmashauri ya Mji Handeni mkoani Tanga, kwa lengo la kupata undani wa migogoro hiyo baada ya kupokea malalamiko.

Hatua hiyo ni sehemu ya juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, za kutafuta suluhu ya kudumu ya migogoro ya ardhi nchini.

Akiwa jijini Tanga tarehe 19 Agosti 2026, Dkt. Akwilapo alianza ziara yake katika eneo la Raskazone ambako alikagua mgogoro unaohusisha Kiwanja Na. 163, Kitalu KB XVI, ambapo mmiliki wake anadai kuwa sehemu ya barabara inayoelekea kwenye ofisi za kampuni ya GBP, imejengwa katika eneo la kiwanja chake. Waziri huyo pia alitembelea eneo la Chumvini, Kata ya Chumbageni, ambako baadhi ya wananchi wanadaiwa kufanya maendelezo ndani ya eneo la hifadhi ya mikoko.

Baadaye, Dkt. Akwilapo alielekea wilayani Handeni na kutembelea maeneo mbalimbali yenye malalamiko ya ardhi katika kata za Kwenjugo, Chanika na Mdoe. Akiwa katika maeneo hayo, alipokea maelezo kutoka kwa madiwani na viongozi wa maeneo husika kuhusu migogoro iliyodumu kwa muda na kusababisha sintofahamu miongoni mwa wananchi, huku akijionea hali halisi ya maeneo yanayolalamikiwa.

Miongoni mwa migogoro aliyoikagua ni ule kati ya Chuo cha Maendeleo ya Wananchi (FDC) cha Handeni na kampuni ya Lyakundi Investment, ambapo kampuni hiyo inadaiwa kumilikishwa eneo lenye ukubwa wa mita za mraba 21,937 badala ya mita za mraba 5,625, hali inayodaiwa kuingia katika eneo linalomilikiwa na chuo hicho.

Dkt. Akwilapo pia alitembelea eneo jirani na Shule ya Msingi Mshikamano, ambako kampuni hiyo ya Lyakundi Investment imezuiwa na Halmashauri ya Mji Handeni kuendeleza kiwanja kufuatia malalamiko ya wananchi na viongozi wao kwamba taratibu za umilikishaji wa eneo hilo hazikuzingatia kanuni.

Katika mwendelezo wa ziara hiyo, Waziri Akwilapo alikagua eneo la Milupi lenye mgogoro kati ya familia ya marehemu Yusuf Ulenge na uongozi wa Mtaa wa Ngugwini kuhusu umiliki wa eneo la ekari 15. Pia alitembelea eneo la Seuta, ambako Diwani wa Kata ya Kwenjugo, Bw. Twaha Mgaya, alieleza kuwa baadhi ya viwanja vimemilikishwa kwa watu bila kufuata taratibu , Waziri pia alitembelea eneo la Kwedisewa.

Eneo jingine alilokagua Dkt. Akwilapo ni lenye mgogoro kati ya Halmashauri ya Mji Handeni na familia ya Hassan Msindo, ambayo inadaiwa kuwa eneo lao la ekari 30 lilipimwa na kugawanywa kuwa viwanja, lakini badala ya familia hiyo kupatiwa asilimia 60 ya eneo inalodai kumiliki, ilipatiwa viwanja vitatu pekee. Familia hiyo imeeleza kutoridhishwa na hatua hiyo na kuiomba Serikali kuingilia kati ili kupatikana suluhu ya haki.

Wakati wa kuhitimisha ziara hiyo Mhe, Dkt Leonard Akwilapo alisistiza umuhimu wa taasisi, viongozi na wananchi kuzingatia Sheria, Kanuni na taratibu za usimamizi na umiliki wa ardhi ili kuzuia migogoro. Hatua hiyo inaendana na moja ya vipaumbele sita vya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi vilivyoainishwa na Waziri huyo wakati wa Bunge la Bajeti 2026/2027, ambacho ni uimarishaji wa mifumo ya utatuzi wa migogoro ya ardhi. 

Aidha aliwapongeza viongozi wa mikoa na wilaya kwa nchi nzima kwa kuisaida wizara katika kushugulikia migogoro ya ardhi katika maeneo yao ya utawala. Waziri alihitimisha kwa kuahidi kutoa maelekezo ya utatuzi wa migogoro aliyiotembelea katika muda mfupi ujao ili wenye haki waendelee na uendelezaji wa maeneo yao.

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo (wa pili kushoto), Mkuu wa wilaya ya Handeni Salum Nyamwese (kushoto) wakioneshwa moja ya eneo lenye mgogoro wa ardhi katika kata ya Chanika kupitia ‘laptop’ na Afisa Ardhi Mwandimizi wa Wizara ya Ardhi Bw. James Balele wakati wa ziara yake wilayani Handeni. Kushoto ni Diwani wa kata ya Chanika Halmashauri ya Mji Handeni Habib Mbota.
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo (wa tatu kushoto) akioneshwa eneo la mgogoro katika kata ya Chanika na Afisa Ardhi Mwandimizi wa wizara ya Ardhi Bw. James Balele wakati wa ziara yake wilayani Handeni. Kulia kwa Waziri ni Mkuu wa wilaya ya Handeni Salum Nyamwese.
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo (Katikati), Mkuu wa wilaya ya HandeniSalum Nyamwese (kushoto) na Diwani wa kata ya Chanika Halamshauri ya Mji Handeni Habib Mbota wakielekea katika moja ya eneo lenye mgogoro wa ardhi wakati wa ziara ya Waziri wilayani handeni jana.Diwani wa Kata ya Kwenjugo Bw, Twaha Mgaya akisisitiza jambo mbele ya Waziri wa Ardh,i Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo alipofanya ziara wilayani Handeni kushughulikia changamoto za migogoro ya ardhi jana.Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo (wa pili kushoto) akioongozwa na Kamishna wa Ardhi Msaidizi mkoa wa Tanga Jabir Singano alipotembelea eneo lenye mgogoro wa ardhi eneo la Raskazone Tanga wakati wa ziara yake mkoani humo jana.Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akioneshwa eneo la Chumvini, Kata ya Chumbageni na Kamishna wa Ardhi Msaidizi mkoa wa Tanga Jabir Singano ambako baadhi ya wananchi wanadaiwa kufanya maendelezo ndani ya eneo la hifadhi ya mikoko (PICHA ZOTE NA WIZARA YA ARDHI).


Na Mwandishi Wetu, Tanga
SERIKALI imesema mashindano ya ujuzi na ubunifu ni sehemu ya mkakati wa kuwaandaa vijana wenye ujuzi unaokidhi mahitaji ya soko la ajira na kuwawezesha kushindana katika majukwaa ya kimataifa.

Hayo ameyasema Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Carolyne Nombo, wakati akizungumza katika Wiki ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu inayoendelea jijini Tanga.

Profesa Nombo amesema Serikali imekuwa ikitumia mbinu mbalimbali kuwawezesha vijana kupata ujuzi, ikiwemo kuwatoa darasani na kuwapeleka katika maeneo halisi ya kazi pamoja na kuwashirikisha katika mashindano yanayopima uwezo na umahiri wao.

Amesema Tanzania baada ya kuwa mwanachama wa mashindano ya WorldSkills, imeanza mchakato wa kuwachagua vijana wenye ujuzi kuanzia ngazi za chini hadi mashindano ya kitaifa, ambapo watakaofanya vizuri wataiwakilisha nchi katika mashindano ya Afrika yanayotarajiwa kufanyika mwaka huu nchini Algeria.

“Tunapotaka kuhamasisha vijana kupata ujuzi, tunatumia mbinu mbalimbali zaidi ya kuwafundisha darasani. Tunataka vijana hawa waende katika maeneo halisi ya kazi ili wapate ujuzi unaotakiwa,” amesema Profesa Nombo.

Amesema vijana wanaoshiriki mashindano hayo wamechaguliwa baada ya kuonyesha umahiri katika fani mbalimbali, huku wataalamu wakifanya tathmini kwa kuzingatia viwango vya kimataifa ili kubaini watakaoiwakilisha Tanzania katika mashindano ya Afrika na baadaye ya dunia.

Profesa Nombo amesema Serikali inalenga kuhakikisha vijana wa Tanzania wanapata fursa ya kuonyesha uwezo wao na kuifanya dunia itambue kuwa nchi ina vijana wenye ujuzi na ubunifu unaoweza kushindanishwa katika majukwaa ya kimataifa.

Amesema Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (NACTVET) limeratibu mashindano hayo kwa kushirikisha wataalamu kutoka ndani na nje ya nchi.

Kwa mujibu wa Profesa Nombo, wataalamu wa Wizara ya Elimu na wadau wengine wamepatiwa mafunzo na wataalamu wa kimataifa kuhusu namna mashindano ya WorldSkills yanavyoendeshwa ili kuhakikisha Tanzania inazingatia vigezo vya kimataifa.

Amesema pia viongozi na wataalamu wa Tanzania watashiriki katika kujifunza namna mashindano ya kimataifa yanavyoandaliwa na kuendeshwa, hatua ambayo itasaidia kuboresha zaidi maandalizi ya timu ya taifa.

Profesa Nombo amesema kinachofurahisha katika mashindano hayo ni ushirikiano unaoendelea kati ya taasisi za elimu, vyuo vya ufundi, viwanda na sekta binafsi katika kuwaandaa vijana.

Amesema wataalamu kutoka sekta binafsi na taasisi mbalimbali wamekuwa wakishirikiana na vyuo kutoa maarifa na uzoefu kwa vijana ili kuwawezesha kufanya vizuri katika mashindano hayo.

“Tunakwenda kwenye mashindano haya kama Tanzania iliyounganika kati ya sekta ya umma na sekta binafsi. Lengo ni kuhakikisha tunashiriki kama timu moja ya Tanzania,” amesema.

Amesema ushirikiano huo ni muhimu kwa kuwa unawawezesha wanafunzi kupata uzoefu wa vitendo na ujuzi unaoendana na mahitaji ya soko la ajira.

Aidha, Profesa Nombo amesema Serikali imeweka mkazo katika elimu jumuishi kwa kuhakikisha vijana wote wanapata fursa ya kutumia vipaji na uwezo wao bila kujali changamoto walizonazo.

Amesema vijana wenye mahitaji maalum wamepewa nafasi ya kushiriki katika mashindano hayo na kuonyesha uwezo wao katika fani mbalimbali.

“Ushiriki wa vijana wenye mahitaji maalum unaonyesha wazi kuwa hata wenye changamoto hizo wanaweza kuwa na mchango mkubwa katika maisha yao na katika maendeleo ya taifa,” amesema.

Amesisitiza kuwa Serikali itaendelea kutoa fursa kwa vijana wote, wakiwemo wenye mahitaji maalum, ili waweze kujenga maisha yao na kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya Taifa.


Na Mwandishi Wetu
WADAU wa teknolojia na usimamizi wa intaneti wametakiwa kutumia fursa zinazotokana na mtandao huo kwa maendeleo ya jamii badala ya kuutumia kwa matusi, chuki, udhalilishaji na vitendo vinavyoweza kuathiri maslahi na haki za watu wengine.

Rai hiyo imetolewa na Mratibu wa Tanzania Internet Governance Forum (TIGF), Dkt. Nazarius Kirama, wakati wa Mkutano wa 13 wa Jukwaa la Usimamizi wa Intaneti Tanzania, unaojadili masuala mbalimbali yanayohusu matumizi, usalama na mustakabali wa intaneti nchini.

Kirama amesema mkutano huo umewakutanisha wadau kutoka serikalini, mashirika yasiyo ya kiserikali, sekta binafsi, wataalamu na wasomi kutoka vyuo vikuu kwa lengo la kujadili namna ya kukuza matumizi salama na yenye tija ya intaneti, huku masuala ya akili mnemba (AI), ujumuishi wa kidijitali, ulinzi wa taarifa binafsi na intaneti yenye kasi yakiwa miongoni mwa mada zinazojadiliwa.

Amesema Jukwaa la Usimamizi wa Intaneti Tanzania lilianza mwaka 2005 na ni sehemu ya mfumo wa mijadala ya usimamizi wa intaneti unaofanyika katika ngazi za kitaifa, kikanda na kimataifa, uliolenga kutoa nafasi kwa wadau kujadili namna bora ya kusimamia mustakabali wa teknolojia hiyo.

Kirama amesema licha ya intaneti kuwa nyenzo muhimu ya kufikisha huduma, taarifa na fursa kwa watu wengi, baadhi ya watumiaji wamekuwa wakiitumia vibaya kwa kutoa lugha za matusi, chuki na vitendo vinavyoweza kuharibu maslahi ya wengine, akisema tabia hizo zinaakisi changamoto zilizopo katika jamii.

“Jamii iliyopo kwenye mitandao ya kijamii haikutoka mbinguni, inatokana na jamii yetu. Kwa hiyo yale mambo yanayofanyika mtaani yanaweza pia kufanyika mtandaoni,” amesema Kirama, huku akiwataka watumiaji kujenga utamaduni wa kujidhibiti badala ya kutegemea udhibiti wa mamlaka pekee.

Amesema wananchi wanapaswa kutafakari thamani wanayoipata kutokana na matumizi ya intaneti na kuhakikisha fedha wanazolipia huduma hiyo zinatumika kwa shughuli zenye manufaa, ikiwamo kujenga jamii, kuelimisha, kuongeza fursa za kiuchumi na kuunganisha watu. “Intaneti ya bure bila faida ni kujiletea umaskini.

Kwa nini utumie fedha kulipia intaneti halafu uitumie kumtukana mtu? Intaneti yenyewe ina gharama,” amesema.

Katika mkutano huo, Mwanaharakati wa masuala ya teknolojia na miundombinu ya TEHAMA, Damilola Kihinde, amewataka wazazi, hospitali na wahusika wengine wanaokusanya au kuhifadhi taarifa za watoto kuhakikisha taarifa hizo zinalindwa ili kuepusha matumizi mabaya, udhalilishaji na uvunjwaji wa haki zao za msingi.

Kihinde amesema mtoto mdogo hawezi kufanya maamuzi kuhusu matumizi ya taarifa zake, hivyo mzazi akiwa mlezi na mlinzi wake wa kwanza ana wajibu wa kuhakikisha picha na taarifa zake hazishirikishwi au kutumiwa kwa namna inayoweza kumletea madhara.

Amesema pia hospitali, ambazo zinaweza kuwa wadhibiti wa taarifa kwa mujibu wa Sheria ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi, zinapaswa kuweka mifumo imara ya kulinda taarifa za watoto na wagonjwa.

Amesisitiza kuwa ulinzi wa taarifa binafsi za watoto ni jukumu la pamoja linalohitaji ushirikiano wa wazazi, hospitali na wahusika wengine, huku maslahi bora ya mtoto na haki yake ya faragha yakipewa kipaumbele.

Kwa upande wake, Pious Sylvester, Mratibu wa Ushirikiano wa Shirika la African Child Project, amesema jamii inapaswa kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa kulinda taarifa za watoto, hasa katika kipindi ambacho matumizi ya mitandao ya kijamii yanaendelea kuongezeka.

Amesema Tanzania pia inapaswa kuendelea kushiriki katika majukwaa ya kikanda na kimataifa kuhusu usimamizi wa intaneti ili kupata fursa ya kujadili changamoto na kutoa mchango katika mijadala ya mustakabali wa teknolojia.




Mkuu wa Chuo cha Bahari Dar es Salaam (DMI), Prof. Tumaini Gurumo, amesema maandalizi ya Kongamano la 5 la Kimataifa la Uchumi wa Buluu yanaendelea vizuri. Kongamano hilo linatarajiwa kufanyika tarehe 7 hadi 9 Septemba 2026 katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNICC), Dar es Salaam, huku washiriki kutoka zaidi ya nchi saba wakitarajiwa kuhudhuria.

Akizungumza na waandishi wa habari leo tarehe 20 Agosti 2026, katika Ukumbi wa Mikutano wa DMI, Prof. Gurumo amesema kongamano hilo limeandaliwa na DMI, chini ya Wizara ya Uchukuzi, kwa kushirikiana na Ofisi ya Makamu wa Rais, likiwa na kaulimbiu “Kuwezesha Shughuli za Uchumi wa Buluu kwa Maendeleo Endelevu ya Afrika.” Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, anatarajiwa kuwa Mgeni Rasmi.

Prof. Gurumo amesema kongamano hilo linafanyika wakati Tanzania ikiendelea na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, huku utajiri wa Bahari ya Hindi, maziwa, mito, visiwa na rasilimali nyingine za maji yakiwa na fursa kubwa katika kuchochea uwekezaji, biashara, ajira, usalama wa chakula, usafiri, utalii, nishati, utafiti na teknolojia.

Ameeleza kuwa kongamano litakuwa jukwaa la kuunganisha tafiti, maarifa, sera, teknolojia na wadau mbalimbali katika kujadili fursa, changamoto na suluhisho za matumizi ya rasilimali za Uchumi wa Buluu kwa maendeleo endelevu. Msisitizo utawekwa katika utafiti na ushahidi wa kisayansi, uwekezaji, ushiriki wa sekta binafsi na wananchi, ubunifu na kujenga uwezo wa kitaasisi, kwa kuzingatia Sera ya Taifa ya Uchumi wa Buluu ya mwaka 2024.

Katika kongamano hilo, wataalamu, watafiti na wanazuoni wanatarajiwa kuwasilisha tafiti na kubadilishana uzoefu katika maeneo mbalimbali, yakiwemo bandari na usafiri wa majini, mazingira ya bahari, mabadiliko ya tabianchi, uvuvi na ufugaji wa viumbe vya majini, sheria za bahari, teknolojia, ujasiriamali, elimu na mafunzo ya bahari, usalama wa bahari na uwekezaji.

Prof. Gurumo amesema kongamano linatarajiwa kuwakutanisha washiriki kutoka Tanzania na mataifa mbalimbali, yakiwemo China, Afrika Kusini, Sweden, Japan, Canada, Russia, Thailand, Morocco, Kenya, Comoro na Uturuki, kwa ajili ya kubadilishana maarifa, teknolojia na uzoefu, pamoja na kuimarisha ushirikiano wa kitaifa, kikanda na kimataifa katika kukabiliana na changamoto za bahari.

Kwa upande wa DMI, Prof. Gurumo amesema kongamano hilo ni sehemu ya jukumu la Chuo la kuwa kitovu cha elimu, mafunzo, utafiti na ubunifu katika sekta ya bahari na Uchumi wa Buluu. Kongamano linatarajiwa kutoa maarifa mapya, mapendekezo ya kisera yanayotokana na ushahidi wa kisayansi, fursa za utafiti na ushirikiano wa kitaaluma na kitaasisi, pamoja na fursa za ubunifu na uwekezaji.

Mkuu wa Chuo cha Bahari Dar es Salaam (DMI), Prof. Tumaini Gurumo, amewakaribisha wataalamu, watafiti, wanazuoni, wawakilishi wa sekta binafsi, wawekezaji, taasisi za kitaifa na kimataifa, wadau wa maendeleo pamoja na jumuiya ya kitaaluma kushiriki katika Kongamano la 5 la Kimataifa la Uchumi wa Buluu, linaloandaliwa na DMI kwa kushirikiana na Ofisi ya Makamu wa Rais na Wizara ya Uchukuzi.




Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Elimu, Utamaduni na Michezo, Mheshimiwa Husna Sekiboko, ametoa wito wa kuimarishwa kwa elimu na mafunzo ya ufundi na ujasiriamali nchini, akisema ujuzi wa vitendo unaweza kuwa silaha muhimu kwa vijana katika kukabiliana na ukosefu wa ajira kwa kujiajiri na kuunda ajira kwa wengine.

Amesema hayo akiwa kwenye banda la VETA katika Maadhimisho ya Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu, Jijini Tanga.

Sekiboko amesema badala ya vijana kuhitimu na kuendelea kusubiri ajira, wanapaswa kutumia ujuzi wanaoupata katika vyuo vya ufundi kuanzisha shughuli za uzalishaji, huku Serikali ikiendelea kuweka mazingira ya kuwawezesha kupata vitendea kazi, mitaji na masoko.

Amesema changamoto ya ukosefu wa ajira inahitaji suluhisho linalowafanya vijana kuwa sehemu ya uzalishaji, akisisitiza kuwa kijana mwenye ujuzi ana uwezo wa kujiajiri na baadaye kuwa mwajiri wa wengine.

“Ni bora kijana kuanza na kile kidogo alichonacho na kujenga shughuli yake mwenyewe, kwa sababu anaweza kujiajiri na baadaye kuajiri wengine. Kwa kufanya hivyo, anakuwa amefanya zaidi kwa ajili yake mwenyewe na jamii yake kuliko kusubiri ajira pekee,” amesema.

Ametoa kauli hiyo baada ya kutembelea banda la VETA na kukutana na vijana na wanachuo na wahitimu wa VETA ambapo amesema ameona uwezo mkubwa walionao katika kutengeneza bidhaa na kutoa huduma zinazoweza kukidhi mahitaji ya jamii.

Kwa mujibu wa Sekiboko, vyuo vya ufundi stadi vina nafasi kubwa katika utekelezaji wa jitihada za kukabiliana na ukosefu wa ajira kwa sababu vinawapatia vijana ujuzi wa vitendo ambao unaweza kutumika moja kwa moja katika uzalishaji.

Amesema ili ujuzi huo uwe na matokeo makubwa zaidi, vijana wanahitaji mazingira mazuri ya kujifunzia, vifaa vya kufanyia kazi na fursa za kupata mitaji ili kugeuza ujuzi wao kuwa biashara na ajira.

Amehimiza vijana kutumia fursa zinazotolewa na Serikali na taasisi mbalimbali kupata ujuzi na mitaji, akisema mtaji mdogo unaweza kuwa mwanzo wa shughuli kubwa endapo utatumika vizuri.

“Lengo ni kuondokana na utamaduni wa kusubiri ajira pekee. Kijana akipata ujuzi, anaweza kuutumia kuzalisha ajira yeye mwenyewe badala ya kusubiri kuajiriwa katika taasisi,” amesema.

Amesema hatua hiyo pia inaweza kusaidia kufikia malengo ya Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 kwa kuongeza idadi ya vijana wanaoshiriki katika uzalishaji na kujenga uchumi kupitia ujuzi, ubunifu na ujasiriamali.









Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Nombo, ameiagiza Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania (TAEC) kuongeza elimu kwa umma kuhusu matumizi ya teknolojia ya nyuklia, ili Watanzania waelewe manufaa yake na matumizi chanya katika maisha na maendeleo ya taifa.

Prof. Nombo ametoa agizo hilo Agosti 20, 2026 jijini Tanga alipotembelea banda la TAEC katika Maonesho ya Wiki ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu Kitaifa yanayofanyika katika viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara kuanzia Agosti 15 hadi 24.

Amesema elimu hiyo ni muhimu katika kuondoa hofu na dhana potofu kuhusu teknolojia ya nyuklia, huku akisisitiza umuhimu wa kuwajengea wananchi uelewa kuhusu matumizi yake katika sekta mbalimbali.

Prof. Nombo amewataka wataalamu wa TAEC kuendelea kujenga uwezo wa wataalamu wengine wa ndani, ili Tanzania iwe na rasilimali watu wenye ujuzi wa kutosha wa kutumia na kuendeleza teknolojia ya nyuklia kwa manufaa ya taifa.

Ameeleza kuwa serikali imeendelea kutoa fursa za masomo na ufadhili (scholarship) kwa Watanzania wanaosomea fani zinazohusiana na teknolojia ya nyuklia, hatua inayolenga kuongeza idadi ya wataalamu wenye ujuzi na kujenga uwezo wa nchi katika eneo hilo.

Aidha, Prof. Nombo amesema Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, anatarajiwa kushiriki katika mkutano wa kimataifa unaohusisha masuala ya teknolojia ya nyuklia ambayo ni ishara ya umuhimu na fursa ya Tanzania kuimarisha ushirikiano na nchi nyingine katika sekta hiyo.

Akizungumza baada ya kupokea maelekezo hayo, Mtafiti Mwandamizi kutoka TAEC, Eng. Christina Paul Nyakyi, amesema taasisi hiyo imepokea maelekezo hayo na itayafanyia kazi kwa kuongeza juhudi za kutoa elimu kwa wananchi kuhusu matumizi salama ya teknolojia ya nyuklia.

Amesema TAEC itaendelea kuweka mkazo katika matumizi ya teknolojia hiyo kwa maendeleo ya taifa, pamoja na kuwaandaa wataalamu wa ndani watakaoweza kushiriki katika matumizi na uendelezaji wa teknolojia ya nyuklia nchini.




 NA EMMANUEL  MASSAKA 

 
MAMLAKA ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA) imeshauriwa kuendelea kuimarisha utoaji wa elimu kwa wananchi kuhusu matumizi sahihi ya dawa na vifaa tiba.Ushauri huo umetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Bi. Queen Sendiga alipokuwa akifungua kikao cha siku mbili kati ya TMDA, wahariri na waandishi wa habari kutoka mikoa ya Manyara, Arusha na Kilimanjaro, kilichofanyika mkoani Manyara.


Lengo la kikao hicho ni kwa kuwajengea uelewa kuhusu majukumu ya TMDA, udhibiti wa dawa, vifaa tiba na vitendanishi pamoja na changamoto zinazojitokeza katika eneo hilo.

Ametumia nafasi hiyo kueleza kuwa taarifa sahihi kuhusu bidhaa za tiba ni muhimu kwa sababu sekta hiyo inahusisha moja kwa moja afya na mustakabali wa jamii, hivyo wananchi wanapaswa kupata taarifa sahihi na kwa wakati ili waweze kufanya maamuzi salama.

Mkuu wa Mkoa huyo amesema wanapozungumzia bidhaa za tiba wanazungumzia afya na mustakabali wa jamii yetu kwa ujumla. Hivyo ni muhimu wananchi wapate taarifa sahihi kuhusu dawa na vifaa tiba.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Dawa za Binadamu na Mifugo wa TMDA, Dkt. Yona Mwalwisi, amesema mamlaka hiyo inaendelea kutekeleza majukumu yake kwa mujibu wa Sheria ya Dawa na Vifaa Tiba, Sura ya 219, inayoiwezesha kusimamia ubora, usalama na ufanisi wa dawa, vifaa tiba na vitendanishi nchini.

“TMDA imejenga utamaduni wa kukutana na wahariri na waandishi wa habari kila mwaka katika maeneo mbalimbali nchini ili kujadili mafanikio, changamoto na mikakati ya pamoja ya kuboresha udhibiti wa bidhaa za tiba na kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu huduma zinazotolewa na mamlaka hiyo.”

Ameongeza utafiti wa kuridhika kwa wananchi na wateja uliofanywa na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, hususan Shule ya Biashara Desemba 2022 katika halmashauri 35 za mikoa 16, umeonesha kuongezeka kwa uelewa kuhusu TMDA kutoka asilimia 47 mwaka 2020, huku kiwango cha kuridhika na huduma za mamlaka hiyo kikiwa asilimia 82.

“Mafanikio hayo yamechangiwa kwa kiasi kikubwa na ushirikiano kati ya TMDA na vyombo vya habari, ambavyo vimekuwa daraja muhimu la kufikisha elimu kwa wananchi kuhusu matumizi sahihi ya dawa na vifaa tiba, pamoja na kuwaelimisha kuhusu hatari za bidhaa bandia, duni na zisizosajiliwa.”

Aidha, amesema TMDA imeendelea kushikilia cheti cha mfumo wa usimamizi wa ubora ISO 9001:2015 pamoja na ithibati ya maabara kwa kiwango cha ISO 17025:2017, jambo linalothibitisha kuwa mifumo na huduma zinazotolewa na mamlaka hiyo zinakidhi viwango vya kimataifa.

Amesema TMDA pia imetambuliwa na Shirika la Afya Duniani (WHO) kuwa mamlaka iliyofikia ngazi ya tatu ya ukomavu wa mifumo ya udhibiti wa bidhaa za tiba, huku ikiendelea na juhudi za kufikia ngazi ya nne, ambayo ndiyo ya juu zaidi, na kuendelea kuwa miongoni mwa mamlaka zinazoongoza barani Afrika.

Pamoja na hayo ameeleza mamlaka hiyo imeimarisha ufuatiliaji wa usalama wa dawa na chanjo baada ya kuingia sokoni, ikiwa ni pamoja na kuongeza vituo vya kufuatilia madhara ya dawa na chanjo hadi kufikia vituo 33 nchini.

Aiidha mtandao wa maabara hamishika ukiongezeka kutoka 19 hadi 28, hatua inayowezesha upimaji wa sampuli katika maeneo mbalimbali kwa wakati. TMDA pia imeweka vituo vya maabara katika vituo vyote 16 rasmi vya forodha vinavyoingiza bidhaa za tiba nchini.



























Top News