Na.Mwandishi wetu - Dar es Salaam

Kamati ya Kitaifa ya Wataalamu ya Usimamizi wa Maafa imeidhinisha Mpango wa Taifa wa Dharura wa Kukabiliana na Madhara ya El Niño na kuzielekeza Wizara, Idara, Taasisi, Mikoa na Halmashauri kuongeza kasi ya maandalizi ili kupunguza madhara yanayoweza kujitokeza kutokana na mvua za El Niño zinazotabiriwa kudumu hadi mwisho wa mwaka 2026.

Akizungumza katika kikao hicho, Mwenyekiti wa Kamati hiyo, ambaye pia ni Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Dkt. Jim Yonazi, ameelekeza kila sekta kutenga rasilimali zitakazowezesha hatua za kuzuia, kujiandaa, kukabili na kurejesha hali katika eneo lake na pia kuandaa mipango ya dharura ya manunuzi. Pia amesisitiza umuhimu wa kutambua mapema maeneo hatarishi, kufanya tathmini za vihatarishi na kuwahamasisha wananchi wanaoishi katika maeneo hayo kuhamia maeneo salama.

Aidha, Dkt. Yonazi ameelekeza wananchi kupewa elimu kuhusu namna ya kupunguza madhara ya mvua hizo kwa kuweka akiba ya chakula, kulima mazao yanayostahimili mvua nyingi na kutumia fursa zitokanazo na mvua katika kilimo, uvunaji wa maji, ufugaji na uvuvi. Vilevile, amezitaka taasisi husika kuandaa mipango ya kuzuia milipuko ya magonjwa kwa binadamu, mifugo na mimea.

Kamati hiyo pia imeagiza ukaguzi na uboreshaji wa miundombinu muhimu ikiwemo barabara, maji na umeme, kuimarisha usimamizi wa mazingira, kuhakikisha vifaa vya uokoaji, huduma za dharura na mifumo ya mawasiliano vinakuwa tayari wakati wote, pamoja na kuhuisha mipango ya utekelezaji katika maeneo hatarishi.

Aidha, Wizara, Taasisi, Mikoa na Halmashauri zimeelekezwa kufuatilia kwa karibu utabiri na maelekezo ya kitaalamu kutoka Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) ili hatua zote za maandalizi na kukabiliana na athari za El Niño zichukuliwe kwa wakati.














 


Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA) imeendelea kutoa elimu na mafunzo kwa vyuo vikuu pamoja na shule za sekondari ikiwa na lengo la kuwajengea ufahamu kuhusu shughuli mbalimbali za Bodi na kukuza Taaluma ya Uhasibu nchini.

Katika kuendeleza jitihada hizo, NBAA imetembelea Chuo Kikuu cha Mzumbe, Kampasi ya Dar es Salaam, tarehe 22 Julai 2026, ambapo ilitoa elimu kwa wanafunzi kuhusu majukumu ya Bodi, fursa zinazopatikana katika Taaluma ya Uhasibu pamoja na taratibu za kuwa Wahasibu na Wakaguzi wa hesabu waliosajiliwa.

Mafunzo hayo yaliwahusisha wanafunzi wa mwaka wa kwanza, wa pili na wa tatu wanaosoma Shahada ya Kwanza ya Uhasibu na Fedha (Bachelor of Accounting and Finance – BAF). Kupitia mafunzo hayo, wanafunzi walipata uelewa kuhusu nafasi ya NBAA katika kusimamia na kuendeleza Taaluma ya Uhasibu na Ukaguzi wa hesabu nchini, pamoja na umuhimu wa kuzingatia maadili, weledi na maendeleo endelevu ya Taaluma.

Akizungumza wakati wa mafunzo hayo, CPA Nicholaus Kishamba, Mkufunzi wa Chuo Kikuu cha Mzumbe, Kampasi ya Dar es Salaam, aliwahimiza wanafunzi kutumia vyema fursa ya elimu wanayoipata chuoni kwa kujiandaa kuwa wataalamu wenye uwezo wa kukidhi mahitaji ya soko la ajira na kuchangia maendeleo ya sekta ya fedha nchini.

Naye Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na Mawasiliano wa NBAA, Magreth Kageya, amesema ziara hiyo imekuwa chachu kwa wanafunzi kwani imewapa fursa ya kupata taarifa mbalimbali kuhusu NBAA, ikiwemo majukumu yake ya kisheria, huduma zinazotolewa na Bodi, taratibu za usajili wa wahasibu na wakaguzi wa hesabu, namna ya kufanya mitihani ya Bodi pamoja na fursa za maendeleo ya Taaluma.

Amesema elimu hiyo inalenga kuwajengea wanafunzi uelewa wa mapema kuhusu Taaluma ya Uhasibu na kuwaandaa kukidhi mahitaji ya soko la ajira mara baada ya kuhitimu masomo yao.

Ziara hiyo pia ilitoa nafasi kwa wanafunzi kuuliza maswali na kupata ufafanuzi kuhusu Taaluma ya Uhasibu, ambapo walihimizwa kujifunza kwa bidii, kuzingatia maadili ya Taaluma na kujiendeleza kitaaluma ili kuwa Wahasibu na Wakaguzi wa hesabu wenye ushindani katika ngazi ya kitaifa na kimataifa.
Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na Mawasiliano wa NBAA, Magreth Kageya akizungumzia kuhusu dhamira ya mafunzo kwa wanafunzi wa mwaka wa kwanza, wa pili na wa tatu wanaosoma Shahada ya Kwanza ya Uhasibu na Fedha (Bachelor of Accounting and Finance – BAF) katika Chuo Kikuu cha Mzumbe , Kampasi ya Dar es Salaam.
Afisa Masoko wa NBAA Salim Kasumari akitoa elimu kuhusu namna ya kufanya mitihani ya Bodi kwa wanafunzi wanaosoma Shahada ya Kwanza ya Uhasibu na Fedha katika Chuo Kikuu cha Mzumbe , Kampasi ya Dar es Salaam.
Mfanyakazi wa NBAA Happiness Mwamwembe akitoa elimu kwa wanafunzi wanaosoma Shahada ya Kwanza ya Uhasibu na Fedha katika Chuo Kikuu cha Mzumbe , Kampasi ya Dar es Salaam.
CPA Nicholaus Kishamba, Mkufunzi wa Chuo Kikuu cha Mzumbe, Kampasi ya Dar es Salaam akitoa neno la shukrani kwa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA) kuendelea kutoa elimu katika chuo hicho.
Baadhi ya wanafunzi wa mwaka wa kwanza, wa pili na wa tatu wanaosoma Shahada ya Kwanza ya Uhasibu na Fedha (Bachelor of Accounting and Finance – BAF) katika Chuo Kikuu cha Mzumbe , Kampasi ya Dar es Salaam wakifuatilia mada zilizokuwa zinatolewa na watumishi wa NBAA waliofika chuoni hapo kutoa elimu.
Baadhi ya watumishi wa NBAA pamoja na mwalimu wa Chuo Kikuu cha Mzumbe wakiwa kwenye picha ya pamoja na wanafunzi wa mwaka wa kwanza, wa pili na wa tatu wanaosoma Shahada ya Kwanza ya Uhasibu na Fedha katika Chuo Kikuu cha Mzumbe , Kampasi ya Dar es Salaam.


NA MWANDISHI WETU, KISARAWE

Kamati ya Utekelezaji ya Baraza Kuu la Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT), imefaya ziara ya mafunzo katika Shirika la Madini la Taifa (STAMICO), Julai 21, 2026, wilayani Kisarawe mkoani Pwani.

Ujumbe huo uliongozwa na Mwenyekiti wa UWT Taifa, Mary Chatanda. Katika ziara hiyo, Wajumbe wa Kamati hiyo, walitembelea kiwanda cha Rafiki Briquettes, kinachochakata makaa ya mawe kuwa nishati safi ya kupikia ambayo ni rafiki wa afya na utunzaji mazingira.

Katika ziara hiyo, Chatanda amesema, wanawake wana mchango mkubwa katika kufanikisha kampeni ya nishati safi ya kupikia kutokana na ukweli kuwa kazi hiyo inafanywa kwa kiwango kikubwa na wanawake.

"Tunamuunga mkono Rais wetu, Dk. Samia Suluhu Hassan, katika kampeni ya kuhimiza matumizi ya nishati safi ya kupikia ili kutunza afya na mazingira. Sisi UWT tunahimiza jamii itumie nishati safi," amesema Chatanda.

Aidha, amesema UWT wapo tayari kuwa mabalozi na kushirikiana na STAMICO katika kutoa elimu kwa wanawake na jamii kwa ujumla ili kuongeza idadi ya watumiaji wa nishati safi nchini.

"UWT tuna vikao na mikutano mingi inayotukutanisha na wanawake na wananchi, hivyo niwaombe wenzetu wa STAMICO watupe wataalamu wa kuja kutoa elimu katika mikusanyiko yetu, ili elimu hiyo iwafikie wananchi wengi zaidi," ameongeza.

Kwa upande wake, Mjumbe wa Kamati hiyo na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Subira Mgallu, ameipongeza STAMICO kwa kusimamia kikamilifu sera ya matumizi ya nishati safi ya kupikia ambayo ni muhimu katika dunia ya sasa ya maendeleo ya sayansi na teknolojia.

Naye, Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe, Petro Magoti, aliwashukuru Wajumbe wa Baraza hilo, kufanya ziara ya mafunzo kwani agenda ya nishati safi ni ya kitaifa na kimataifa, hivyo wakawe mabalozi wa kuelimisha wengine watumie nishati hiyo.








Mkurugenzi wa TAWA TZ Engineering and Heaters Limited, Tawaqal Hassan, amesema kampuni hiyo imeshiriki Jukwaa la Tano la Utekelezaji wa Ushirikishwaji wa Watanzania katika Sekta ya Madini (LCCF 2026) linalofanyika jijini Mwanza kutokana na ubora wa bidhaa zake, hususan hita zinazotumika katika uchenjuaji wa madini. 

Akizungumza na waandishi wa habari Julai 22, 2026, alisema vifaa hivyo vina mchango mkubwa katika kuongeza ufanisi wa upatikanaji wa dhahabu wakati wa uchenjuaji wa madini, huku akieleza ubora wa hita zinazozalishwa na kampuni hiyo unapimwa kwa kuzingatia viwango, voltage inayozalishwa, pamoja na uimara wa bidhaa hizo na wamekuwa wakipokea maoni chanya kutoka kwa wateja na wadau wanaotumia bidhaa zao.

Kwa mujibu wa Hassan, TAWA TZ Engineering and Heaters Limited inajihusisha na utengenezaji wa hita kwa matumizi ya migodini, viwandani, mahoteli, Bekari, viwanda vinavyohitaji joto katika uzalishaji, pamoja na vifaa vya kuyeyusha lami, amesema bidhaa hizo zimetengenezwa kwa kuzingatia mahitaji ya soko na kutoa suluhisho la kudumu kwa watumiaji.

Aidha, amesema serikali imewawezesha wao Kama vijana kupitia utoaji wa vibali vya kutengeneza bidhaa hizo nchini, hatua ambayo imewapa fursa ya kuonyesha uwezo wao wa ubunifu na uzalishaji, ameongeza kuwa kampuni ipo tayari kuhudumia wateja wote wanaohitaji bidhaa hizo na inaendelea kujivunia kuwa miongoni mwa kampuni ya kwanza ya  Kitanzania kutengeneza hita za aina hiyo kwa viwango vya ubora.

Hassan amesema wateja wakuu wa kampuni hiyo ni sekta ya madini, huku akieleza kuwa ushiriki wao katika LCCF 2026 utawapa nafasi ya kujenga ushirikiano na wadau kutoka ndani na nje ya nchi, pia ametoa wito kwa Watanzania kuendelea kutumia bidhaa zinazozalishwa nchini ili kuunga mkono juhudi za wazawa, kukuza viwanda vya ndani na kuchochea maendeleo ya uchumi. 



Mwambata wa ubalozi  wa Oman nchini Tanzania, Abdulrahman Salim Algaad akiwa na familia yake, ametembelea Hifadhi ya Ngorongoro  na kushuhudia maajabu ya utalii yaliyopo katika kivutio namba moja cha utalii barani afrika

Akimpokea mwambata huyo, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi anayesimamia Huduma za Utalii na Masoko  Mariam  Kobelo ameeleza kuwa jitihada za mamlaka hiyo kuwafikia wadau mbalimbali zimeendelea kuzaa matunda ambapo watumishi kutoka balozi mbalimbali ndani na nje ya nchi wamendelea kutembelea hifadhi hiyo.

 Akiwa ndani ya hifadhi hiyo, Abdulrahman Algaad na familia yake walipata fursa ya kushuhudia wanyamapori adimu wakiwa katika mazingira yao ya asili, wanyamapori wakubwa watano, misitu, maporomoko ya maji, urithi wa utamaduni na mambo kale, makumbusho ya urithi geopark na kueleza kuwa ndoto na hisia alizokuwa nazo zimekutana na uhalisia.

 Mwambata huyo ameonyesha kuvutiwa na uzuri wa Hifadhi ya Ngorongoro na vivutio vya utalii vilivyopo Tanzania na kupongeza hatua za uhifadhi zinazofanyika na kuifanya Ngorongoro kuendelea kuheshimika kimataifa na kuwa eneo la urithi wa dunia lenye hadhi tatu za kimataifa.

 Kwa upande wake, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi anayesimamia huduma za utalii na masoko, Mariam Kobelo amebainisha kuwa ziara za viongozi na maafisa wa kidiplomasia wanaotembelea Ngorongoro zinachangia kuitangaza Tanzania kimataifa, kuimarisha ushirikiano katika sekta ya utalii, kuongeza ushirikiano kupitia diplomasia ya uchumi.






NA FARIDA MANGUBE MOROGOGO

Mradi wa kuongeza uwezo wa kusimamia Sera za Uchumi Jumuishi (IGE) umechangia Tanzania kuimarisha ukuaji wa uchumi, uundaji wa ajira na usimamizi endelevu wa mazingira kwa kuunganisha watafiti na watunga sera katika kutatua changamoto za maendeleo.

Mradi huo unaofadhiliwa na Shirika la Maendeleo la Sweden (Sida) unatekelezwa katika Nchini za Tanzania, Uganda, Kenya, Rwanda na Ethiopia kwa lengo la kuimarisha sera za uchumi jumuishi zinazochochea maendeleo bila kuathiri mazingira.

Msimamizi Mkuu wa mradi huo nchini Tanzania kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dkt. Aloyce Hepelwa, amesema mradi umefanikiwa kuziba pengo lililokuwepo kati ya watafiti na watunga sera kwa kuwashirikisha katika kufanya tafiti na kuchambua changamoto zinazozuia ukuaji wa uchumi ili kupata suluhisho la pamoja.

Dkt. Hepelwa amesema kupitia Shule Kuu ya Uchumi ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, mradi unasaidia matumizi endelevu ya rasilimali za asili ikiwemo maji, misitu, madini na kilimo ili kuongeza tija ya uchumi huku ukilinda mazingira. Ameeleza kuwa ushirikiano huo umewezesha tafiti kutumika moja kwa moja katika kuboresha sera na maamuzi ya Serikali yanayolenga maendeleo endelevu.

Kwa upande wake, Mtafiti Mwandamizi kutoka Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), Mhandisi Dkt. Befrina Igulu, amesema taasisi hiyo imekuwa ikishirikiana na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam katika kufanya tafiti zinazosaidia utekelezaji wa programu za uhifadhi wa mazingira na usimamizi wa rasilimali za asili kwa ufanisi zaidi.

Naye Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Usimamizi wa Mazingira katika Wizara ya Kilimo, Dkt. Rose Mbezi, amesema licha ya changamoto zinazosababishwa na mabadiliko ya tabianchi, sekta ya kilimo bado ni mhimili wa uchumi wa nchi nyingi za Afrika na pia imeendelea kutoa fursa mpya za maendeleo. Amesema takribani asilimia 70 ya Waafrika hutegemea kilimo kwa maisha yao, hivyo sera zinazochochea uchumi jumuishi na matumizi endelevu ya rasilimali ni muhimu katika kukuza uchumi na kuhimili athari za mabadiliko ya tabianchi.







Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, akiwasili katika ukumbi wa mikutano, jijini Accra, Ghana kwa ajili ya kushiriki Mkutano Maalum wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika (AU) kuhusu Afya, tarehe 22 Julai, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na Rais wa Jamhuri ya Ghana, Mhe. John Dramani Mahama, kabla ya ufunguzi wa Mkutano Maalum wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika (AU) kuhusu Afya, unaofanyika jijini Accra, tarehe 22 Julai, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na viongozi mbalimbali kwenye Mkutano Maalum wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika (AU) kuhusu Afya, jijini Accra, Ghana, tarehe 22 Julai, 2026.




 

Meneja Rasilimali Watu wa Mgodi wa Geita Gold Mining Limited (GGML), Dominick Marandu, amesema kampuni hiyo imeendelea kuwa kinara katika ushirikishwaji wa Watanzania kwenye sekta ya madini kupitia ajira, manunuzi na utekelezaji wa miradi ya maendeleo ya jamii, amesema GGML imekuwa mshiriki na mdhamini wa Jukwaa la Utekelezaji wa Ushirikishwaji wa Watanzania katika Sekta ya Madini (LCCF) tangu lilipoanzishwa.

Akizungumza na waandishi wa habari Julai 22, 2026, wakati wa ufunguzi wa Jukwaa la Tano la LCCF jijini Mwanza, Marandu amesema kampuni hiyo inaamini rasilimali za madini zinapaswa kuwanufaisha Watanzania pamoja na jamii zinazozunguka maeneo ya migodi, amesisitiza kuwa ushirikishwaji wa wananchi ni sehemu muhimu ya maendeleo ya sekta hiyo.

Amesema GGML imefanikiwa kuwaajiri Watanzania kwa kiwango kikubwa, ambapo asilimia 98 ya wafanyakazi wake ni wazawa wenye taaluma na ujuzi mbalimbali wanaoshiriki katika shughuli za uzalishaji, na hatua hiyo inalenga kujenga uwezo wa wataalamu wa ndani na kuongeza mchango wao katika uchumi wa taifa.

Marandu pia ameeleza kuwa kampuni hiyo inaendelea kutoa kipaumbele kwa wazawa katika manunuzi, akibainisha kuwa asilimia 97 ya manunuzi yaliyofanyika katika nusu ya kwanza ya mwaka 2026 yalifanywa kupitia kampuni za Watanzania, ambapo GGML inafanya kazi kwa karibu na Tume ya Madini kuhakikisha sheria za maudhui ya ndani zinazingatiwa kikamilifu.

Aidha, kupitia programu ya Graduate, amesema zaidi ya wahitimu 300 wa vyuo vikuu wamenufaika katika kipindi cha miaka saba iliyopita kwa kupata mafunzo ya vitendo yanayowawezesha kupata uzoefu wa kazi, huku baadhi yao wakiajiriwa pindi nafasi zinapopatikana, aidha kampuni inaendelea kutekeleza takribani miradi 60 ya Uwajibikaji na urejeshaji kwa Jamii (CSR) katika maeneo yanayozunguka mgodi.

Marandu amewahimiza Watanzania, hususan vijana, kutumia fursa zinazotolewa na GGML kupitia ajira, mafunzo na utoaji wa huduma mbalimbali, amesema ushiriki wa wazawa katika sekta ya madini ni msingi wa kuongeza tija, kukuza uchumi na kuhakikisha rasilimali za nchi zinawanufaisha wananchi.



Na Benny Mwaipaja, London.


Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (MB), ameanza ziara ya kikazi ya siku sita jijini London, Uingereza, ambapo atashiriki katika matukio mbalimbali ikiwemo kuwa Mgeni Rasmi katika uzinduzi wa hatifungani ya kwanza ya nje yenye sarafu ya Shilingi ya Tanzania inayotolewa na Shirika la Fedha la Kimataila (IFC) katika Soko la Hisa la London

Hatifungani hiyo inatarajiwa kupanua fursa za uwekezaji nchini na kuvutia aina mpya za wawekezaji wa kimataifa ambao wataunga mkono ajenda ya maendeleo ya muda mrefu ya nchi.

Mhe. Balozi Omar alipowasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Heathrow, alilakiwa na Mwenyeji wake, Balozi wa Tanzania nchini Uingereza, Mhe. Balozi Mbelwa Kairuki, ambaye baadae Alasiri, alimkaribisha katika Ofisi za Ubalozi wa Tanzania Jijini London ambapo alipokea taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya Ubalozi na baadae kujadili ajenda za ziara hiyo.

Ziara ya Mheshimiwa Balozi Omar inayoanza leo tarehe 21 hadi 26 Julai 2026, inalenga kuimarisha ushiriki wa Tanzania katika masoko ya kimataifa ya fedha, kuvutia mitaji ya muda mrefu na kuithibitisha nchi kama moja ya maeneo yanayovutia zaidi uwekezaji barani Afrika.

Ziara hiyo pia inatoa fursa ya kufanya majadiliano na wasimamizi wa mali wa kimataifa, wawekezaji wa serikali, taasisi za uwekezaji wa maendeleo na benki za biashara kuhusu fursa zilizopo katika miundombinu, nishati, viwanda, kilimo, madini na huduma za kifedha.

Aidha, atashiriki mazungumzo ya pande mbili na washirika mbalimbali wa maendeleo na taasisi kubwa za kifedha duniani ikiwemo Benki ya Dunia, Shirika la Fedha la Kimataifa (IFC), Standard Bank na Soko la Hisa la London, kuhusu mwelekeo wa uchumi wa nchi, Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050 pamoja na Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Miaka Mitano (FYDP IV).















Top News