Na Mwandishi Wetu, Tanga
MKURUGENZI Mkuu wa Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA), CPA Anthony Kasore, amesema mamlaka hiyo imeweka mkakati wa kutoa mafunzo ya ufundi na ujuzi kwa vijana ili kuwafungulia fursa za ajira na kujiajiri katika sekta mbalimbali.

CPA Kasore ameyasema hayo alipotembelea Banda la VETA katika Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu inayoendelea katika Viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara jijini Tanga.

Amesema VETA ina vyuo katika mikoa mbalimbali nchini, hivyo vijana wanapaswa kutumia fursa hiyo kujiunga na vyuo hivyo na kupata ujuzi unaowawezesha kukabiliana na mahitaji ya soko la ajira.

“VETA imejenga vyuo katika kila mkoa na wilaya zake kwa kuzingatia mahitaji ya wananchi wa maeneo husika, ili kuhakikisha changamoto zao zinapatiwa ufumbuzi kupitia elimu na mafunzo ya ufundi stadi,” amesema CPA Kasore.

Aidha, amesema gharama za mafunzo kwa wanafunzi wanaosoma kozi ndefu ni Sh 60,000 kwa mwaka kwa wanafunzi wa kutwa, huku wanafunzi wa bweni wakilipia Sh 120,000 kwa mwaka.

Amesema gharama hizo zimewekwa ili kuwawezesha vijana wengi kupata fursa ya elimu na mafunzo ya ufundi stadi bila kukwamishwa na gharama kubwa.

CPA Kasore amesema kupitia vyuo vyake, VETA imekuwa ikikuza ubunifu katika sekta mbalimbali kwa lengo la kutatua changamoto zinazowakabili wananchi pamoja na kurahisisha shughuli zao katika mazingira bora.

Amesema ubunifu huo ni sehemu ya juhudi za VETA kuhakikisha vijana wanapata ujuzi unaoendana na mahitaji ya sasa na kuwawezesha kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi, ajira na kujiajiri.



Na Mwandishi Wetu, Tanga
WANAFUNZI wa Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere (MNMA) wamebuni mifumo ya kidijitali inayolenga kurahisisha usimamizi wa taka na matumizi ya maji kwa kutumia teknolojia ya mawasiliano.

Mwanafunzi wa Fani ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (ICT), Fatuma Ismail, amebuni mfumo unaowezesha vifaa vya kuhifadhi taka kutoa taarifa kwenye simu janja pindi taka zinapofikia kiwango cha kujaa, hivyo kurahisisha hatua za kuziondoa.

Akizungumza katika Banda la MNMA kwenye Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu inayoendelea katika Viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara jijini Tanga.

Fatuma amesema mfumo huo unalenga kusaidia katika utunzaji wa mazingira na kudumisha usafi.

Amesema mfumo huo unaweza kutumiwa katika maeneo mbalimbali, ikiwemo majumbani, kwa kufungwa kwenye vifaa vya kuhifadhi taka ili kutoa taarifa kwa njia ya simu janja pindi taka zinapokuwa zimejaa.

Fatuma amesema mfumo huo pia unaweza kusaidia Baraza la Taifa la Usimamizi na Uhifadhi wa Mazingira (NEMC) kufuatilia hali ya maeneo ya kuhifadhi taka na kupata taarifa kwa wakati ili kuchukua hatua stahiki.

Amesema matumizi sahihi ya mfumo huo yanaweza kupunguza msongamano wa taka katika maeneo mbalimbali kutokana na kuwepo kwa mawasiliano ya moja kwa moja kati ya kifaa cha kuhifadhi taka na mtumiaji.

Kwa upande mwingine, mbunifu wa MNMA, Godfrey Kasembe, amebuni kifaa kinachoweza kufungwa kwenye mita za maji na kutoa taarifa za matumizi ya maji moja kwa moja kwenye simu janja au kompyuta bila mhusika kwenda kusoma mita hizo.

Kasembe amesema MNMA imekuwa ikimsimamia kwa karibu katika hatua zote za ubunifu huo, kuanzia wazo hadi kufikia hatua ya kutengeneza kifaa.

Amesema mfumo huo utasaidia mamlaka za maji kupunguza gharama na muda unaotumika kwa watumishi kwenda nyumba kwa nyumba kusoma mita, kwa kuwa taarifa za matumizi zitapatikana moja kwa moja kupitia mfumo huo.

Ameongeza kuwa teknolojia hiyo pia itasaidia kupunguza uwezekano wa udanganyifu katika usomaji wa mita kwa kuwa taarifa za matumizi zitakuwa zikiwasilishwa moja kwa moja kwenye mfumo. Kasembe amesema kwa sasa mfumo huo upo katika hatua za usajili ili kukamilisha taratibu na kuanza kutumika.



Na Mwandishi Wetu, Tanga
CHUO cha Elimu ya Biashara (CBE) kimesema kimeweka mfumo wa kuwawezesha wanafunzi kuendeleza mawazo na bunifu zinazolenga kutoa suluhisho kwa changamoto zinazowakabili wananchi.

Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Masoko wa CBE, Georgina Misama, amesema hayo kwenye Banda la chuo hicho katika Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu inayoendelea jijini Tanga.

Amesema kupitia wiki hiyo, CBE imekuwa ikitoa elimu kwa wananchi pamoja na kuonyesha bunifu mbalimbali zinazozalishwa na wanafunzi, huku chuo kikiwasimamia wanafunzi kuanzia hatua ya awali ya wazo hadi kukamilika kwa bunifu hizo.

“Chuo kimekuwa na mfumo wa kuendeleza bunifu na mawazo yanayotolewa na wanafunzi ambayo yana lengo la kutatua changamoto zinazowakabili wananchi,” amesema Georgina.

Kwa upande wake, mwanafunzi wa mwaka wa tatu wa CBE, Amiri Sharifu, amebuni kifaa cha kidijitali kwa ajili ya wakaguzi wa mizani, kinachowawezesha kupata taarifa za mizani wanayoikagua moja kwa moja kupitia simu zao za mkononi.

Amesema mfumo huo unalenga kuondoa changamoto ya wakaguzi kutembea na vitabu vya karatasi nyingi wakati wa kujaza taarifa za ukaguzi wa mizani, huku pia ukipunguza muda unaotumika katika zoezi hilo.

“Kwa kutumia mfumo huu, mkaguzi anaweza kupata taarifa za mzani papo hapo kupitia simu yake ya mkononi bila kutegemea karatasi, jambo ambalo litasaidia kupunguza muda wa ukaguzi,” amesema Sharifu.

Naye mwanafunzi wa mwaka wa kwanza, Sambu Timothy, amebuni mfumo wa kidijitali unaojulikana kama Smart Mauzo, unaomsaidia mfanyabiashara kupata taarifa za mauzo ya biashara yake kupitia simu janja.

Amesema mfumo huo una uwezo wa kutambua wateja ambao hawajafanya manunuzi kwa muda mrefu na kuwawezesha wafanyabiashara kuwatumia ujumbe mfupi wa simu (SMS) ili kuwakumbusha kuhusu bidhaa au huduma zao.

Timothy amesema mfumo huo upo katika hatua za mwisho za kukamilishwa na baada ya hapo utaingizwa sokoni kwa lengo la kuwasaidia wafanyabiashara kutunza kumbukumbu za uwekezaji, mauzo na matumizi, hatua ambayo itawasaidia kukuza biashara zao.





Na Mwandishi Wetu, Tanga
MAMLAKA ya Elimu Tanzania (TEA) imesema mdau yeyote atakayechangia katika Mfuko wa Elimu wa Taifa, ataweza kupata fursa ya kuomba nafuu ya kodi kwa kutumia cheti cha utambuzi kinachotolewa na mamlaka hiyo.

Akizungumza katika Banda la TEA kwenye Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu inayoendelea katika Viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara jijini Tanga, Afisa Mwandamizi wa TEA Joyce Minja amesema, wachangiaji wa Mfuko wa Elimu hupata manufaa mbalimbali kutokana na mchango wao katika kuendeleza sekta ya elimu.

Amesema miongoni mwa manufaa hayo ni kutambuliwa kwa mchango wao, kupata fursa ya kuomba nafuu ya kodi pamoja na kutangazwa ndani na nje ya nchi kama sehemu ya kuhamasisha wadau wengine kushiriki katika maendeleo ya elimu.

“Wachangiaji wa Mfuko wa Elimu wa Taifa, watapewa Cheti au Barua ya utambuzi wa uchangiaji elimu katika kusaidia maendeleo na uboreshaji miundombinu ya sekta ya elimu,” amesema Minja.

Ameongeza kuwa, cheti hicho kinaweza kutumika katika kuomba nafuu ya kodi kwa mujibu wa Kifungu cha 16(1) cha Sheria ya Kodi ya Mapato, Sura ya 332, Toleo la 2019.

Aidha, amesema wachangiaji wataingizwa katika kanzidata ya wachangiaji wa Mfuko wa Elimu, hatua itakayosaidia kutunza kumbukumbu zao kwa kudumu na kuwezesha kutambua mchango walioutoa katika sekta ya elimu.

Kwa mujibu wa TEA, wachangiaji pia watapata fursa ya kutambuliwa na kutangazwa ndani na nje ya nchi, ikiwa ni sehemu ya kuhamasisha ushiriki wa wadau katika kusaidia maendeleo ya elimu.

Mfuko wa Elimu wa Taifa unalenga kuimarisha ushiriki wa wadau mbalimbali katika maendeleo ya sekta ya elimu kupitia michango na misaada inayolenga kuboresha mazingira na huduma za elimu nchini.

Amewataka wadau mbalimbali ,wakiwemo wafanyabiashara ,wenye viwanda ,Taasisi za Serikali, Sekta Binafsi mashirika ya ndani na nje ya nchi kuendelea kuunga mkono juhudi za Serikali za kuboresha miundombinu ya kujifinzia na kufundishia kwa kuchangia rasilimali fedha au vifaa kupitia Mfuko huo wa Elimu wa Taifa
Na OSCAR ASSENGA, Tanga
SERIKALI imezindua programu ya InnoIP Tanzania, inayolenga kuwasaidia zaidi ya wabunifu 5,000 nchini kulinda kazi zao kisheria, kuzigeuza kuwa fursa za biashara na kuchochea uundaji wa ajira.

Programu hiyo pia inalenga kukabiliana na changamoto ya wizi wa mawazo na ubunifu inayowakabili wabunifu wengi, hasa wanaoweka wazi mawazo yao kabla ya kuchukua hatua za kuyakinga kisheria.

Uzinduzi huo umefanywa Agosti 22, 2026, na Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mhe. Balozi Dkt. Batilda Burian, katika maadhimisho ya Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu yanayoendelea katika Viwanja vya Usagara, jijini Tanga.


Akizungumza na mamia ya wadau wa sekta ya sayansi na ubunifu, Dkt. Batilda alisema Tanzania inapaswa kuhakikisha ubunifu wa ndani unalindwa kisheria na kuunganishwa na masoko makubwa ili kuongeza thamani ya bidhaa na teknolojia zinazozalishwa na Watanzania.

Alisema baadhi ya wabunifu hupoteza fursa kwa kuweka wazi mawazo yao mapema bila kuwa na makubaliano yanayoeleweka kuhusu umiliki wa ubunifu huo

Kwa mujibu wa Dkt. Batilda, hali hiyo inaweza kumsababishia mbunifu kukosa ulinzi wa kisheria wa kazi yake na kuwafanya wawekezaji kusita kuwekeza katika kampuni changa ambazo hazina uthibitisho wa umiliki wa haki zao za miliki bunifu.



Sambamba na uzinduzi wa InnoIP Tanzania, Mkuu wa Mkoa alitangaza kuanza kwa programu ya Fursa Women, inayolenga kuwawezesha wanawake wajasiriamali kutumia teknolojia na mifumo ya kidijitali kukuza biashara zao.

Dkt. Batilda alisema matumizi ya teknolojia yanaweza kupunguza gharama za uendeshaji wa biashara na kuwawezesha wafanyabiashara kuwafikia wateja wengi kwa haraka zaidi.

Aidha, alizitaka vyuo vikuu na taasisi za utafiti kuhakikisha tafiti zinazofanyika zinageuzwa kuwa bidhaa na suluhisho halisi zinazowanufaisha wananchi, badala ya kuishia kwenye makabrasha na makabati.


Pia aliwataka wawekezaji na taasisi za fedha kushirikiana na wabunifu wa Kitanzania kwa kununua bidhaa zao, kuwekeza katika teknolojia zao na kuwawezesha kupata mitaji kwa ajili ya kukuza biashara.

Akizungumzia ushiriki wa Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA), Mkurugenzi wa Miliki, Loy Mhando, aliyemwakilisha Afisa Mtendaji Mkuu, alisema InnoIP Tanzania haimaanishi kuwa kila ubunifu lazima upatiwe hataza (Patent).

Alisema programu hiyo itawasaidia wabunifu kutambua aina sahihi ya ulinzi wa kisheria kulingana na aina ya ubunifu wao, ikiwemo hataza, alama za biashara, hakimiliki na siri za biashara.

Alifafanua kuwa InnoIP inasimamiwa na BRELA na kuratibiwa na Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH), kupitia atamizi za Dar Teknohama Business Incubator (DTBi) na Buni Innovation Hub.

Programu hiyo inalenga kuwasaidia kampuni changa, watafiti, wanafunzi wa vyuo vikuu, biashara ndogo na za kati pamoja na wajasiriamali kutambua, kulinda na kubiasharisha haki zao za miliki bunifu.

Mhando alisema katika mwaka wa kwanza wa utekelezaji, programu hiyo inalenga kufanya uchambuzi wa kina wa mahitaji ya wabunifu 120 wa awali, ambao watasaidiwa kisheria na kifedha kulinda kazi zao na baadaye kuunganishwa na wawekezaji.

Alisema uteuzi wa wabunifu hao utazingatia vigezo mbalimbali, ikiwemo umuhimu wa ubunifu husika kwa jamii pamoja na uwezo wake wa kuzalisha faida.

Kwa mujibu wa Mhando, programu hiyo itawasaidia wabunifu kupitia hatua saba: utambuzi na uhamasishaji; mafunzo na warsha za vitendo; uchambuzi wa mahitaji; maandalizi ya ramani ya ulinzi; uwasilishaji wa maombi ya usajili; ubiasharishaji kwa kuwaunganisha na wawekezaji; pamoja na ufuatiliaji endelevu.

Aliwataka wabunifu na kampuni changa kutumia fursa hiyo mapema badala ya kusubiri hadi mgogoro wa umiliki unapotokea, mawazo yao yanaponakiliwa au mwekezaji anapohitaji uthibitisho wa kisheria kuhusu umiliki wa biashara.



Naye Mkurugenzi Mkuu wa COSTECH, Dkt. Amos Nungu, alisema miliki bunifu si suala la kisheria pekee, bali ni rasilimali muhimu ya kiuchumi inayoweza kuwa msingi wa kuvutia uwekezaji, utoaji wa leseni kwa viwanda vingine, uhamishaji wa teknolojia na ujenzi wa biashara zinazoweza kukua hadi masoko ya kimataifa.

“Changamoto yetu kuu kwa sasa nchini si ukosefu wa mawazo; ni kuhakikisha kuwa mawazo mazuri ya vijana, watafiti na wabunifu wetu yanalindwa kisheria, yanaendelezwa na hatimaye yanafikishwa sokoni,” alisema Dkt. Nungu.

Alisema mafanikio ya InnoIP hayatapimwa kwa idadi ya watu watakaohudhuria mafunzo na semina pekee, bali kwa matokeo, ikiwemo kuongezeka kwa idadi ya ubunifu unaolindwa kisheria, teknolojia mpya kuingia sokoni, biashara kukua, uwekezaji kuvutiwa na ajira mpya kuzalishwa.

Akizungumzia programu ya Fursa Women, Dkt. Nungu aliishukuru Airtel Tanzania kwa kushirikiana na COSTECH katika kufadhili programu hiyo.

Alisema ushirikiano huo unaonesha umuhimu wa sekta ya umma na binafsi kufanya kazi kwa pamoja katika kujenga jamii yenye ujuzi wa kidijitali.

Alifafanua kuwa kupitia Fursa Women, wanawake watajengewa uelewa kuhusu matumizi sahihi na salama ya mifumo ya kidijitali katika kutangaza bidhaa, kuwafikia wateja, kufanya na kupokea malipo mtandaoni pamoja na kuhifadhi kumbukumbu za biashara zao.

Dkt. Nungu alitoa wito kwa wawekezaji na sekta binafsi kutambua kuwa ubunifu wa Kitanzania ni fursa ya uwekezaji ambayo bado haijatumika kikamilifu.

Aliwaalika kushirikiana na Serikali katika kujaribu, kununua na kupanua matumizi ya teknolojia pamoja na suluhisho mbalimbali zinazozalishwa na Watanzania.

Maonesho ya Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu yanatarajiwa kufungwa Jumatatu na Waziri Mkuu, Mhe. Mwigulu Nchemba.
Shule zinazomilikiwa na taasisi na wawekezaji binafsi zimetakiwa kuimarisha ushirikiano wa kitaaluma na kijamii baina yao pamoja na shule za Serikali, huku zikitumia ushindani wa kiushindani kama chachu ya kuboresha viwango vya elimu na kukuza maendeleo ya wanafunzi.

Wito huo umetolewa na Diwani wa Kata ya Kwembe katika Halmashauri ya Manispaa ya Ubungo, Mkoa wa Dar es Salaam, Bw. Kawina Hadji Konde, alipokuwa mgeni rasmi katika mahafali ya saba ya Shule ya Awali na Msingi ya Mwendo, iliyopo Kibamba kwa Mangi, wilayani Ubungo.

Akizungumza katika hafla hiyo iliyowakutanisha wazazi, walimu, wanafunzi na wadau mbalimbali wa elimu, Bw. Konde alisema shule binafsi na zile za Serikali zina nafasi kubwa ya kujenga mifumo ya ushirikiano katika maeneo mbalimbali, ikiwemo elimu, michezo, sanaa, utamaduni na shughuli za kijamii, kwa lengo la kubadilishana uzoefu na kuinua viwango vya elimu kwa manufaa ya wanafunzi na jamii kwa ujumla.

Alisema ushindani kati ya shule unapaswa kujengwa katika misingi chanya inayochochea ubunifu, ubora wa ufundishaji na ujifunzaji, badala ya kuwa kikwazo cha ushirikiano kati ya taasisi hizo.

“Kwenye hili niwapongeze sana uongozi wa Shule ya Mwendo kupitia Mkuu wa Shule, Mwalimu Adolf Nyabarimba, ambaye kwa kweli amekuwa mdau mkubwa na mzuri katika masuala mbalimbali yanayohusu Kata yetu ya Kwembe. Amekuwa akishiriki vikao na mikutano mbalimbali inayohusiana na kata yetu kila anapohitajika na amekuwa akitoa ushirikiano wakati wote. Huu ni mfano wa kuigwa kwa viongozi wa shule nyingine, kwa sababu shule ni sehemu ya jamii,” alisema Bw. Konde.

Aidha, Bw. Konde aliwasisitiza wazazi kuongeza ushirikiano na walimu katika malezi ya watoto, akieleza kuwa elimu bora haiishii darasani pekee, bali inahitaji pia misingi imara ya maadili, uwajibikaji, uzalendo na malezi yenye mwelekeo chanya.

Aliwataka wazazi na walezi kuwa karibu zaidi na watoto wao, kuwafuatilia na kuwasaidia kukabiliana na changamoto mbalimbali za kijamii zinazoweza kuathiri ustawi wao wa kimwili na kisaikolojia, huku akisisitiza umuhimu wa kujenga mazingira salama kwa watoto ndani na nje ya shule.

Kwa upande wake, uongozi wa Shule ya Mwendo ulieleza umuhimu wa ushirikiano kati ya shule, wazazi na jamii katika kuhakikisha wanafunzi wanapata elimu inayowaandaa kuwa raia wenye maarifa, nidhamu, ubunifu na uwezo wa kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya taifa.

Mahafali hayo yalipambwa na burudani na maonesho mbalimbali yaliyoandaliwa na wanafunzi, yakiwemo muziki, sanaa, utamaduni, ukakamavu pamoja na maonesho ya kitaaluma, yaliyowapa wazazi na wageni fursa ya kushuhudia vipaji na uwezo wa wanafunzi nje ya masomo ya darasani.

Diwani wa Kata ya Kwembe, Halmashauri ya Manispaa ya Ubungo, Mkoa wa Dar es Salaam, Bw. Kawina Hadji Konde (wa pili kulia), akimkabidhi Manal Salum, mwanafunzi wa darasa la saba, zawadi ya Mwanafunzi Bora wa Kike katika Shule ya Awali na Msingi ya Mwendo, iliyopo Kibamba kwa Mangi, Wilaya ya Ubungo, wakati wa hafla ya mahafali ya saba ya shule hiyo, yaliyofanyika mwishoni mwa wiki. Wanaoshuhudia tukio hilo ni viongozi na walimu wa shule hiyo.

Diwani wa Kata ya Kwembe, Halmashauri ya Manispaa ya Ubungo, Mkoa wa Dar es Salaam, Bw. Kawina Hadji Konde (wa tatu kulia), akimkabidhi Olivia Kassim, mwanafunzi wa elimu ya awali, cheti cha kuhitimu elimu hiyo katika Shule ya Awali na Msingi ya Mwendo, iliyopo Kibamba kwa Mangi, Wilaya ya Ubungo, wakati wa hafla ya mahafali ya saba ya shule hiyo, yaliyofanyika mwishoni mwa wiki. Wanaoshuhudia tukio hilo ni viongozi na walimu wa shule hiyo.




Mahafali hayo yalipambwa na burudani na maonesho mbalimbali yaliyoandaliwa na wanafunzi, yakiwemo muziki, sanaa, utamaduni, ukakamavu pamoja na maonesho ya kitaaluma, yaliyowapa wazazi na wageni fursa ya kushuhudia vipaji na uwezo wa wanafunzi nje ya masomo ya darasani.

Katika mahafali hayo, walimu, wazazi na wanafunzi walipata wasaa wa kucheza pamoja ili kujipongeza kwa hatua hiyo muhimu.



 



Na OSCAR ASSENGA, Tanga

SERIKALI imezindua programu ya InnoIP Tanzania, inayolenga kuwasaidia zaidi ya wabunifu 5,000 nchini kulinda kazi zao kisheria, kuzigeuza kuwa fursa za biashara na kuchochea uundaji wa ajira.

Programu hiyo pia inalenga kukabiliana na changamoto ya wizi wa mawazo na ubunifu inayowakabili wabunifu wengi, hasa wanaoweka wazi mawazo yao kabla ya kuchukua hatua za kuyakinga kisheria.

Uzinduzi huo umefanywa Agosti 22, 2026, na Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mhe. Balozi Dkt. Batilda Burian, katika maadhimisho ya Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu yanayoendelea katika Viwanja vya Usagara, jijini Tanga.

Akizungumza na mamia ya wadau wa sekta ya sayansi na ubunifu, Dkt. Batilda alisema Tanzania inapaswa kuhakikisha ubunifu wa ndani unalindwa kisheria na kuunganishwa na masoko makubwa ili kuongeza thamani ya bidhaa na teknolojia zinazozalishwa na Watanzania.

Alisema baadhi ya wabunifu hupoteza fursa kwa kuweka wazi mawazo yao mapema bila kuwa na makubaliano yanayoeleweka kuhusu umiliki wa ubunifu huo

Kwa mujibu wa Dkt. Batilda, hali hiyo inaweza kumsababishia mbunifu kukosa ulinzi wa kisheria wa kazi yake na kuwafanya wawekezaji kusita kuwekeza katika kampuni changa ambazo hazina uthibitisho wa umiliki wa haki zao za miliki bunifu.


Sambamba na uzinduzi wa InnoIP Tanzania, Mkuu wa Mkoa alitangaza kuanza kwa programu ya Fursa Women, inayolenga kuwawezesha wanawake wajasiriamali kutumia teknolojia na mifumo ya kidijitali kukuza biashara zao.

Dkt. Batilda alisema matumizi ya teknolojia yanaweza kupunguza gharama za uendeshaji wa biashara na kuwawezesha wafanyabiashara kuwafikia wateja wengi kwa haraka zaidi.

Aidha, alizitaka vyuo vikuu na taasisi za utafiti kuhakikisha tafiti zinazofanyika zinageuzwa kuwa bidhaa na suluhisho halisi zinazowanufaisha wananchi, badala ya kuishia kwenye makabrasha na makabati.

Pia aliwataka wawekezaji na taasisi za fedha kushirikiana na wabunifu wa Kitanzania kwa kununua bidhaa zao, kuwekeza katika teknolojia zao na kuwawezesha kupata mitaji kwa ajili ya kukuza biashara.

Akizungumzia ushiriki wa Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA), Mkurugenzi wa Miliki, Loy Mhando, aliyemwakilisha Afisa Mtendaji Mkuu, alisema InnoIP Tanzania haimaanishi kuwa kila ubunifu lazima upatiwe hataza (Patent).

Alisema programu hiyo itawasaidia wabunifu kutambua aina sahihi ya ulinzi wa kisheria kulingana na aina ya ubunifu wao, ikiwemo hataza, alama za biashara, hakimiliki na siri za biashara.

Alifafanua kuwa InnoIP inasimamiwa na BRELA na kuratibiwa na Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH), kupitia atamizi za Dar Teknohama Business Incubator (DTBi) na Buni Innovation Hub.

Programu hiyo inalenga kuwasaidia kampuni changa, watafiti, wanafunzi wa vyuo vikuu, biashara ndogo na za kati pamoja na wajasiriamali kutambua, kulinda na kubiasharisha haki zao za miliki bunifu.

Mhando alisema katika mwaka wa kwanza wa utekelezaji, programu hiyo inalenga kufanya uchambuzi wa kina wa mahitaji ya wabunifu 120 wa awali, ambao watasaidiwa kisheria na kifedha kulinda kazi zao na baadaye kuunganishwa na wawekezaji.


Alisema uteuzi wa wabunifu hao utazingatia vigezo mbalimbali, ikiwemo umuhimu wa ubunifu husika kwa jamii pamoja na uwezo wake wa kuzalisha faida.

Kwa mujibu wa Mhando, programu hiyo itawasaidia wabunifu kupitia hatua saba: utambuzi na uhamasishaji; mafunzo na warsha za vitendo; uchambuzi wa mahitaji; maandalizi ya ramani ya ulinzi; uwasilishaji wa maombi ya usajili; ubiasharishaji kwa kuwaunganisha na wawekezaji; pamoja na ufuatiliaji endelevu.

Aliwataka wabunifu na kampuni changa kutumia fursa hiyo mapema badala ya kusubiri hadi mgogoro wa umiliki unapotokea, mawazo yao yanaponakiliwa au mwekezaji anapohitaji uthibitisho wa kisheria kuhusu umiliki wa biashara.




Naye Mkurugenzi Mkuu wa COSTECH, Dkt. Amos Nungu, alisema miliki bunifu si suala la kisheria pekee, bali ni rasilimali muhimu ya kiuchumi inayoweza kuwa msingi wa kuvutia uwekezaji, utoaji wa leseni kwa viwanda vingine, uhamishaji wa teknolojia na ujenzi wa biashara zinazoweza kukua hadi masoko ya kimataifa.

“Changamoto yetu kuu kwa sasa nchini si ukosefu wa mawazo; ni kuhakikisha kuwa mawazo mazuri ya vijana, watafiti na wabunifu wetu yanalindwa kisheria, yanaendelezwa na hatimaye yanafikishwa sokoni,” alisema Dkt. Nungu.

Alisema mafanikio ya InnoIP hayatapimwa kwa idadi ya watu watakaohudhuria mafunzo na semina pekee, bali kwa matokeo, ikiwemo kuongezeka kwa idadi ya ubunifu unaolindwa kisheria, teknolojia mpya kuingia sokoni, biashara kukua, uwekezaji kuvutiwa na ajira mpya kuzalishwa.


Akizungumzia programu ya Fursa Women, Dkt. Nungu aliishukuru Airtel Tanzania kwa kushirikiana na COSTECH katika kufadhili programu hiyo.

Alisema ushirikiano huo unaonesha umuhimu wa sekta ya umma na binafsi kufanya kazi kwa pamoja katika kujenga jamii yenye ujuzi wa kidijitali.

Alifafanua kuwa kupitia Fursa Women, wanawake watajengewa uelewa kuhusu matumizi sahihi na salama ya mifumo ya kidijitali katika kutangaza bidhaa, kuwafikia wateja, kufanya na kupokea malipo mtandaoni pamoja na kuhifadhi kumbukumbu za biashara zao.

Dkt. Nungu alitoa wito kwa wawekezaji na sekta binafsi kutambua kuwa ubunifu wa Kitanzania ni fursa ya uwekezaji ambayo bado haijatumika kikamilifu.

Aliwaalika kushirikiana na Serikali katika kujaribu, kununua na kupanua matumizi ya teknolojia pamoja na suluhisho mbalimbali zinazozalishwa na Watanzania.

Maonesho ya Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu yanatarajiwa kufungwa Jumatatu na Waziri Mkuu, Mhe. Mwigulu Nchemba.

 

Mkuu wa Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela Mhe. Omari Issa atunuku shahada za umahiri na uzamivu kwa wahitimi 138 katika Mahafali ya 12 ya Taasisi ya Nelson Mandela yaliyofanyika Leo tarehe 20 Agosti 2026, NM-AIST Tengeru Arusha.

Mwenyekiti wa Baraza la Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela (NM-AIST), Balozi Maimuna Tarishi, amesisitiza umuhimu wa kuhakikisha tafiti, teknolojia na ubunifu unaozalishwa na Taasisi unatafsiriwa kuwa bidhaa, huduma na suluhisho halisi kwa changamoto za jamii, sambamba na utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Tanzania 2050.

Akizungumza katika Mahafali ya 12 ya Taasisi (NM-AIST), Balozi Tarishi amesema ubunifu haupaswi kuishia kwenye makaratasi au usajili wa hati miliki, bali unapaswa kutumika kutatua changamoto katika sekta za kilimo, ufugaji, biashara, mazingira na uchumi.

“Ubunifu usiishie kwenye makaratasi wala usajili BRELA; twende tukautafsiri kwa vitendo ili kujibu changamoto mbalimbali za jamii,” amesema Balozi Tarish.

Aidha, amewataka wahitimu kutumia maarifa na ujuzi walioupata NM-AIST kujitolea kuitumikia jamii ya Tanzania na Afrika, badala ya kutumia elimu kwa manufaa binafsi pekee.

Kwa upande wake, Makamu Mkuu wa NM-AIST, Prof. Maulilio Kipanyula, amesema jumla ya wahitimu 138 wamehitimu katika mahafali hayo, wakiwa wamezalisha machapisho 219 ya kisayansi na hati miliki saba.

Amesema NM-AIST itaendelea kuhamasisha wanafunzi na watafiti kuzalisha bidhaa, kufanya ugunduzi na kuchapisha tafiti katika majarida ya kimataifa. 

Pia, Profesa Maulilio Kipanyula amesema watafiti 19 wa NM-AIST wametambuliwa katika tuzo za Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia zinazohusisha machapisho katika majarida ya kisayansi yenye hadhi ya juu duniani.

NM-AIST inaendelea kubadili maarifa kuwa ubunifu, ubunifu kuwa bidhaa na huduma, na tafiti kuwa suluhisho la changamoto za jamii sambamba na utekelezaji wa Dira 2050.

Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa, Idara ya Mambo ya Siasa na Uhusiano wa Kimataifa (SUKI), Ndugu Rabia Abdalla Hamid (MCC), amewasisitiza wananchi wa Mkoa wa Pwani kuendelea kulinda amani, utulivu na mshikamano wa Taifa, akieleza kuwa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kitaendelea kusimamia jitihada za kuboresha na kustawisha maisha ya kila Mtanzania.

Ndugu Rabia amesema kila Mtanzania ni sehemu ya historia na maendeleo ya Tanzania, hivyo ana wajibu wa kulinda amani, umoja na utulivu wa nchi kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Ametoa kauli hiyo leo, Agosti 23, 2026, wakati akiendelea na ziara yake katika Mkoa wa Pwani yenye lengo la kusikiliza makundi mbalimbali ya kijamii, kubaini changamoto zinazowakabili na kutafuta namna bora ya kuzitatua.

Katika ziara hiyo, Ndugu Rabia amekutana na kuzungumza na makundi mbalimbali, yakiwemo viongozi wa dini, wazee, wakulima, wafugaji, mashirika yasiyo ya kiserikali (NGOs), umoja wa wasusi, wafanyabiashara, wanamichezo, wavuvi, wanavyuo, walimu, Machinga, Mawinga, Mama Lishe, Baba Lishe, vyama vya ushirika, umoja wa mashamba ya chumvi, wajane, wachimbaji wa madini, maafisa usafirishaji pamoja na vikundi mbalimbali vya ujasiriamali.

Amesema CCM itaendelea kusikiliza wananchi na kufuatilia changamoto zao kwa lengo la kuhakikisha jitihada za maendeleo zinagusa makundi mbalimbali na kuboresha maisha ya wananchi.

Ndugu Rabia amesisitiza kuwa ushirikiano kati ya wananchi na Serikali ni muhimu katika kujenga Tanzania yenye amani, umoja na maendeleo endelevu.

















Top News