Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea Tanzania (TFRA) Kanda ya Kaskazini imetumia Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu jijini Tanga kuelimisha wananchi kuhusu matumizi sahihi ya mbolea, ubunifu wa kiteknolojia pamoja na fursa za mbolea ya ruzuku kwa wakulima.
Akizungumza na Michuzi Tv Agosti 18, 2026 katika viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara jijini Tanga, Meneja wa TFRA Kanda ya Kaskazini, Gothard Liampawe, amesema TFRA imejipanga kutumia mashamba ya mfano kuwafundisha wakulima matumizi sahihi ya mbolea ili kuongeza uelewa na tija katika uzalishaji.
Amesema pamoja na elimu kupitia mashamba ya mfano, TFRA imebuni mifumo mbalimbali ya kiteknolojia inayorahisisha utekelezaji wa majukumu yake, ikiwemo Mfumo wa FIS, unaomwezesha mfanyabiashara kujisajili na kuomba leseni ya biashara, kusajili mbolea na kupata vibali vya kusafirisha au kuingiza mbolea nchini bila kufika katika ofisi za TFRA.
“Mfanyabiashara anaweza kutumia kompyuta yake akiwa mahali popote alipo kufanya maombi hayo bila kulazimika kufika ofisini, hivyo tunaokoa muda na gharama za usafiri,” amesema Liampawe.
Amesema ubunifu huo umeipa TFRA fursa ya kushiriki katika Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu jijini Tanga, kwa lengo la kuwaonesha Watanzania hatua iliyofikiwa katika matumizi ya teknolojia na namna inavyoweza kurahisisha huduma mbalimbali.
Liampawe amesema kuelekea msimu mpya wa kilimo, TFRA Kanda ya Kaskazini imejipanga kuimarisha huduma kwa wakulima na watoa huduma katika sekta ya mbolea kwa kuwatembelea wadau na kuhakikisha wanapata huduma bora, huku ikipanua wigo wa elimu kupitia kampeni ya “Mali Shambani, Silaha Mbolea.”
Amesema katika mwaka wa 2025/2026, Kanda ya Kaskazini imesimamia utekelezaji wa mpango wa mbolea za ruzuku ambapo zaidi ya wakulima 650,000 wamejisajili na kuwa tayari kunufaika na mpango huo, huku wakulima 173,000 tayari wakiwa wamenufaika na jumla ya tani 179,000 za mbolea hadi wiki iliyopita.
Ameutaja mkoa wa Kilimanjaro kuwa kinara kwa matumizi ya mbolea za ruzuku katika Kanda ya Kaskazini, ukifuatiwa na Arusha, Manyara na Tanga, huku zaidi ya Shilingi bilioni 80 zikiwa zimetumika katika upatikanaji wa mbolea hizo.
Aidha, Liampawe amewahimiza wakulima ambao tayari wamejisajili kutotumia vibaya fursa hiyo ya ruzuku inayotolewa na Serikali, huku ambao hawajajisajili akiwataka kufanya hivyo ili waweze kunufaika na mpango huo na kuongeza tija katika kilimo.


.jpeg)



.jpeg)






.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)
















.jpeg)

.jpeg)



.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)





