Taasisi ya INADES Formation Tanzania imeadhimisha Siku ya Mazingira Duniani kwa kupanda miti 200 ya kivuli na matunda katika Shule ya Sekondari Kisima cha Ndege iliyopo Wilaya ya Bahi mkoani Dodoma.

Zoezi hilo ni sehemu ya mwendelezo wa kampeni ya “Panda Mti Tuilinde Kesho” iliyozinduliwa Januari 2026, yenye lengo la kuchangia juhudi za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi na kuimarisha utunzaji wa mazingira.

Akizungumza baada ya shughuli ya upandaji miti iliyofanyika Juni 5, 2026, Mwakilishi wa INADES Formation Tanzania, Paul Ephras Chugu, amesema taasisi hiyo imefanikiwa kupanda miti zaidi ya 15,000 katika vijiji vinne vya Wilaya ya Bahi tangu kuanza kwa kampeni hiyo.

Kwa upande wake, Afisa Mazingira wa Halmashauri ya Wilaya ya Bahi, Joyce Anania Jackson, ameipongeza INADES Formation Tanzania kwa ushirikiano mzuri unaoendelea kati ya taasisi hiyo na halmashauri katika kutekeleza shughuli za uhifadhi wa mazingira.

Naye Mkuu wa Shule ya Sekondari Kisima cha Ndege,  Mwalimu wa Mazingira na Mwenyekiti wa Klabu ya Mazingira wa shule hiyo, wamepongeza juhudi za taasisi hiyo kwa kuendelea kutoa elimu na kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa utunzaji wa mazingira.

Maadhimisho hayo ya Siku ya Mazingira Duniani yaliambatana na bonanza la michezo lililowakutanisha wanafunzi wa shule hiyo, wanafunzi kutoka shule jirani pamoja na wananchi wa vijiji vya jirani, kwa lengo la kutoa elimu kuhusu uhifadhi wa mazingira na kuhamasisha ushiriki wa jamii katika kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.







WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali itaendelea kusimamia utoaji wa haki kwa wananchi na kuimarisha uwajibikaji kwa watumishi wa umma ili kuhakikisha huduma za Serikali zinatolewa kwa ufanisi, kwa wakati na kwa kuzingatia maslahi ya wananchi.

Amesema hayo leo Ijumaa, Juni 5, 2026 alipokuwa akizungumza na kusikiliza kero za wananchi wa Halmashauri ya Wilaya ya Iringa katika Jimbo la Isimani mkoani Iringa katika viwanja vya Isimani tarafani.

Dkt. Mwigulu amesema haki za wananchi hazipaswi kucheleweshwa wala kunyimwa kwa sababu yoyote na kusisitiza kuwa kila anayestahili haki yake anapaswa kuipata kwa mujibu wa sheria na taratibu zilizowekwa.

“Haki si hisani. Tunataka anayestahili haki apewe haki yake. Serikali haitavumilia vitendo vya kupora au kuchelewesha haki za wananchi kwa sababu yoyote ile,” amesema.

Aidha, Waziri Mkuu amesema watumishi wa umma wanapaswa kutambua kuwa nafasi walizonazo ni dhamana ya kuwatumikia wananchi na kwamba huduma zinazoweza kutolewa kwa siku hiyo zinapaswa kutolewa bila kuwazungusha wananchi.

“Linaloweza kufanyika leo lifanyike leo. Wananchi wanapofika katika ofisi za umma wanapaswa kuhudumiwa kwa heshima, haraka na kwa ufanisi,” amesema.

Pia amesema Serikali itaendelea kuchukua hatua kali dhidi ya watumishi watakaobainika kushindwa kutekeleza majukumu yao ipasavyo, hususan wale wanaokwaza utoaji wa huduma na matumizi sahihi ya rasilimali za umma.

Waziri Mkuu amesema uwajibikaji, uadilifu na utoaji wa huduma bora ni msingi muhimu wa kujenga imani ya wananchi kwa Serikali na kuhakikisha maendeleo yanawafikia wananchi wote.

Kadhalika, amewahakikishia wananchi wa Isimani kuwa Serikali itaendelea kutekeleza ahadi zilizotolewa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na miradi ya maendeleo iliyopo kwenye Ilani ya Chama Cha Mapinduzi kwa lengo la kuboresha maisha ya wananchi.









Na Jawadu Kinyobwa - Dsm

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete amewataka Wanafunzi wa sheria kujenga taaluma zao katika misingi ya nidhamu, ubunifu na uzalendo ili waweze kufanikiwa katika soko la ajira la kimataifa linalozidi kuwa na ushindani.

Akizungumza leo Juni 5, 2026 katika hafla ya Siku ya Kazi na Taaluma ya Shule ya Sheria ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, amesema mafanikio ya kitaaluma hayawezi kupatikana bila kuzingatia maadili hayo matatu muhimu.

Akifafanua kuhusu nidhamu, amesema ubora si jambo la muda mfupi bali ni tabia inayojengwa kwa kujifunza kwa bidii, kutunza muda, kuwa na hamu ya kujifunza mambo mapya na kuzingatia maadili ya taaluma. 

Amefafanua kuwa, nidhamu inayojengwa kupitia mahakama za mfano, kazi za kitaaluma na shughuli za msaada wa kisheria ndiyo msingi wa kukabiliana na changamoto za taaluma katika ngazi za kitaifa na kimataifa.

Aidha, kuhusu ubunifu, Waziri huyo amesema maendeleo ya teknolojia yamebadili kwa kiasi kikubwa namna taaluma ya sheria inavyotekelezwa duniani. Ametaja matumizi ya Akili Mnemba, mifumo ya kidijitali ya usajili na teknolojia za kisheria kuwa miongoni mwa mabadiliko yanayounda upya mazingira ya kazi za sheria. 

Katika hatua nyingine, amesisitiza umuhimu wa uzalendo, akieleza kuwa wao ni walinzi wa utawala wa sheria na utawala bora hivyo wanapopata fursa ya kufanya kazi  katika taasisi za kimataifa au kampuni kubwa nje ya nchi, wanapaswa kutumia maarifa na uwezo wao kuisaidia Tanzania kutambulika vyema nje ya nchi.

Sambamba na hayo, Amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuimarisha sekta ya sheria na haki kupitia mageuzi ya mfumo wa haki, matumizi ya teknolojia, uwekezaji katika miundombinu ya utoaji haki na kuhamasisha mifumo mbadala ya utatuzi wa migogoro.

Awali, akizungumzia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Mhe. Ridhiwani amesema sekta ya sheria ni nguzo muhimu katika kuharakisha maendeleo ya kiuchumi na kijamii kupitia mchango wa wataalamu wa sheria katika kulinda maslahi ya taifa, kuimarisha utawala wa sheria na kusaidia mageuzi ya kidijitali.

Na Beda Msimbe,TBN, Moscow

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk Samia Suluhu Hassan amesema wakati umefika kwa Tanzania na Urusi kutekeleza makubaliano na kuacha maneno katika kufanikisha makubaliano yanayokuza biashara na uwekezaji.

Amesema kwamba uwekezaji Tanzania unalipa hasa katika mikakatik ambayo imelenga kutekeleza Dira ya maendeleo ya 2050.

Alisema kwamba milango ya Tanzania ipo wazi kuona kwamba makubaliano ya ujenzi wa viwanda vya dawa, viua dud una uwekezaji kwimngine unfanyuiwa kazi kwa manjufaa ya pande zote mbili.

Alisema ikiwa sehemu ya kurahisha utekelezaji wa mikataba ya uwekezaji kuanzia Julai 2 mwaka huu Shirika la Ndege (ATCL) litaanza safari za moja kwa moja kutoka Dar es Salaam, Moscow na Zanzibar.

Aidha ni matarajio ya Rais Samia kwamba Shirika la Ndege la Urusi la Azur pia litanza safari hizo.

Akizungumza na wafanyabiashara juu ya nafasi ya wananchi wa pande zote mbili kunufaika na uhusiano huo, Rais Samia alizungumzia kuhusu uwekezaji wa Urusi nchini Tanzania na kuwaita wafanyabuashara na wawekezaji katika nishati, madini, dawa za binadamu, viwatilifu na kilimo na kusema mabadiliko makubwa yanatakiwa kufanywa ili kupunguza urari wa biashara.

Alisema kwamba ujazo wa sasa biashara hauakisi ukweli kuwa kuna nafasi kubwa ya kuwapo kwa maendeleo ya ushirikiano hasa katika n yajna ambazo ni za kimkakati zinazolenga kuihudumia Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050.

Naye Waziri wa Maendeleo ya Kiuchumi wa Urusi, Maxim Reshetnikov amesema kwamba amefurahishwa na juhudi za kuifungua Tanzania zinazofanywa na Rais Samia Suluhu Hassan.

Alisema juhudi hizo zinazaa matunda na kwamba Urusi ipo tayari kushirikiana na Tanzania katika miradi yake ya kimkakati.

Anasema taifa hilo litaendelea kufungua fursa mbalimbali kwa kuwekeza nchini Tanzania katika kilimo na teknolojia na viwanda

“Tanzania ni lango la mashariki ya kati tupo tayari kuwapatia teknolojia na utaalamu wetu na tupo tayari kushiriki katika kuanzisha viwanda mbalimbali vya dawa na mbolea” alisisitiza waziri huyo akishukuru kwa namna ambavyo wafanyabiashara wa Tanzania walivyofika kwa wingi baada ya mkutano wa Arusha, kushiriki katika ukamilishaji wa mambo mbalimbali.

Aidha mmoja wa wafanyabiashara wa Kitanzania akizungumza baada ya kukamilika kwa kongamano hilo, Dhruv Jog, amesema kualikwa kwa wafanyabiashara katika safari ya Rais na kushiriki kongamano hilo inaonesha ni kwa namna gani sekta binafsi inathaminiwa katika kubadili maisha ya Watanzania.

Alisema kitendo hicho kinasaidia kuifungua jumuiya ya sekta binafsi katika daraja jingine. Alisema kufanikiwa kufungua soko la Urusi kutawezesha watanzania kufanya biashara na nchi takribani 15 zinazofanya ukanda wa Urusi hivyo kuleta kipato zaidi.

Katika ziara hii ya kihistoria ikifanywa kwa mara ya pili katika historia ya uhusiano wa Tanzania na Urusi, ya kwanza ilikuwa ni miaka ya 1960 iliyofanywa na baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere, Rais Samia anaendeleza kampeni kubwa ya kuhakikisha Tanzania inanufaika pia kiuchumi na uhusiano mzuri na mataifa mbalimbali.

Akiwa hapa Rais Samia alifanya mazungumzo na Rais Vladmir Putin katika lengo la kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia, kisiasa, kiuchumi na kihistoria baina ya Tanzania na Urusi

Pia Rais Samia ameiweka Tanzania katika ramani ya uwekezaji kwa hotuba yake aliyoitoa katika mkutano mkubwa wa uwekezaji jijini St Petersburg.








Spika Zungu Aonya Matumizi ya Lugha za Kudhalilisha Bungeni, Kauli ya Mbunge Lucy Mayenga Kufutwa HansadNa Janeth Raphael MichuziTv - Bungeni Dodoma

Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mussa Azan Zungu, amesisitiza umuhimu wa wabunge kuzingatia kanuni, sheria na maadili ya Bunge kwa kuepuka matumizi ya lugha za matusi au kauli zinazoweza kuwadhalilisha wabunge wenzao wakati wa mijadala ya kibunge.

Akiongoza shughuli za Bunge leo Spika Zungu ameeleza kuwa kauli iliyotolewa na Mbunge Lucy Mayenga ya kusema kuwa “mbunge Sigrada Mligo (CHAUMA) hajitambui” ni kauli ya kuudhi na yenye kudhalilisha mbunge mwingine, jambo ambalo halikubaliki ndani ya chombo hicho cha juu cha kutunga sheria.

Amesema kuwa matumizi ya lugha zisizofaa yanakiuka kanuni za Bunge na yanaweza kuathiri hadhi na heshima ya mijadala ya kitaifa inayofanyika ndani ya ukumbi wa Bunge.

Kutokana na tukio hilo, Spika Zungu alitoa onyo kali kwa wabunge wote, akiwataka kujiepusha na kauli zinazoweza kuleta mvutano au kudhalilisha wenzao, huku akisisitiza kuwa nidhamu na heshima ni msingi muhimu wa uendeshaji wa shughuli za kibunge.

Aidha, aliamuru kauli hiyo iliyotolewa na Mbunge Lucy Mayenga iondolewe kwenye hansadi rasmi za Bunge kwa kuwa imeonekana kwenda kinyume na taratibu na maadili ya chombo hicho.

Katika hatua nyingine, Spika Zungu aliwataka wabunge kuendelea kuzingatia sheria, kanuni na maadili ya kibunge ili kulinda heshima ya Bunge na kuhakikisha mijadala inafanyika kwa ustaarabu na kwa maslahi ya taifa.

Awali, Spika huyo alimwapisha rasmi Mbunge mpya wa Jimbo la Isimani, Emanuela Mtafikikolo Kaganda, ambaye amechukua nafasi iliyoachwa wazi kufuatia kifo cha aliyekuwa Mbunge wa jimbo hilo, William Lukuvi.


Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi ametoa wito wa kutumia Maadhimsho ya Siku ya Mazingira Duniani kukumbuka wajibu wa kuunganisha nguvu katika jitihada za kuhifadhi mazingira, na kuhakikisha matumizi adili ya rasilimali nyingi ambazo Tanzania imejaaliwa kuwa nazo.

Makamu wa Rais ametoa wito huo, alipomwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani, ambayo Kitaifa yamefanyika katika Kituo cha Mikutano cha Jakaya Kikwete mkoani Dodoma.

Amesema baadhi ya mambo muhimu ya kuzingatia katika uhifadhi wa mazingira ni pamoja na kuendelea kutoa elimu kwa umma kuhusu masuala ya mazingira na kuimarisha mfumo wa usimamizi wa taka hususan katika Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa dhana ya uchumi rejeshi, kwa kuwa maeneo mengi bado hali ya usafi haridhishi.

Makamu wa Rais ameongeza kwamba, ni vema kuendelea kubadili mtazamo ili kuziona taka kama fursa ya kiuchumi na kuzitumia kutengeneza bidhaa mbalimbali kama vile mbolea, chakula cha mifugo na bidhaa nyinginezo. Hali kadhalika, kuendelea kutekeleza Mkakati wa Taifa wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia ambapo hadi sasa, matumizi hayo yameendelea kuimarika kutoka 6.9% mwaka 2021 hadi kufikia 28.6% mwaka 2025.

Aidha, Makamu wa Rais amehimiza kuongezwa kwa jitihada za uhifadhi na utunzaji wa mazingira ambapo ameagiza Mamlaka zinazotoa vibali vya ujenzi kuweka sharti na kusimamia ili kila kibali cha ujenzi kinachotolewa kinaambatana na agizo la kupanda miti isiyopungua mitano pamoja na kuzielekeza Mamlaka za Serikali za Mitaa hususan Manispaa na Majiji kuazisha Bustani za kijani na kuhakikisha zinatunzwa ipasavyo.

Pia Makamu wa Rais ameagiza Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania kuhakikisha uwepo wa miche ya miti ya kutosha ili kurahisisha na kuwezesha zoezi la upandaji miti nchini, Mamlaka husika kuimarisha udhibiti wa uharibifu wa maeneo yote yanayopandwa miti pamoja na kuiagiza Ofisi ya Makamu wa Rais kupitia kituo cha Taifa cha kuratibu kaboni kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI), kubainisha misitu inayofaa na kuisajili katika biashara ya kaboni.

Vilevile, Makamu wa Rais ametoa rai kwa Taasisi za utafiti kufanya tafiti kuhusu mimea au viumbe vamizi ambavyo vinazidi kuongezeka na kuathiri mifugo na mimea mingine katika maeneo mbalimbali nchini. Pia ameagiza Mamlaka za Serikali za Mitaa kuimarisha mifumo ya usimamizi wa taka hususan kuanzisha vituo vya kuchakata taka ili kupunguza kiasi cha taka katika madampo na kuchagiza urejelezaji.

Makamu wa Rais ametoa wito kwa kila mwananchi kuwajibika kuhakikisha kwamba suala la utunzaji na usafi wa mazingira, ikiwemo udhibiti wa taka linapewa kipaumbele. Amesema ni vema kutambua suala la ulinzi na uhifadhi wa mazingira halina mbadala, kwa kuwa mazingira ndiyo uhai na uchumi.

Kwa upande wake, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhandisi Hamad Masauni, amesema Uzinduzi wa Programu ya Mageuzi ya Kimkakati ya Mazingira Endelevu Tanzania, itakayotekelezwa kwa kipindi cha miaka mitano (2026 – 2030), imelenga kuchochea matokeo makubwa ya haraka katika kurejesha uoto wa asili, kuimarisha ustawi wa mfumo wa ikolojia pamoja na kutoa huduma za kiikolojia ambazo ni msingi muhimu wa uzalishaji katika sekta mbalimbali za uchumi.

Amesema hatua hizo zitaweza kuchangia katika kufanikisha malengo ya Dira 2050 ambayo inalenga kuifanya nchi kuwa na ustawi wa mazingira na ustamilivu mkubwa wa mabadiliko ya tabianchi. Ameongeza kwamba Programu hiyo, inalenga kuhamasisha upandaji wa miti bilioni mbili kila mwaka, kuongeza matumizi ya nishati safi ya kupikia, kuimarisha usimamizi wa taka, kukuza biashara ya kaboni pamoja na kuongeza ushiriki wa wananchi hususani wanawake na vijana katika uchumi wa kijani.

Maadhimisho hayo, yaliobebwa na kauli mbiu isemayo, “Dira 2050: Tuwajibike Kukijanisha Tanzania” yamehudhuriwa na wadau mbalimbali wa mazingira wa Kitaifa na Kimataifa, Viongozi mbalimbali, Wanafunzi na Wananchi.








 Na Mwandishi Wetu

Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) inaandaa mapendekezo ya  kufanya maboresho ya  Kanuni za Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229, ili kuwezesha wahitimu wa taaluma za Habari, Uhusiano na Mawasiliano kwa Umma kupata ithibati bila sharti la kuwasilisha barua ya mwajiri.

Hayo yamesemwa leo tarehe 05 Juni, 2026 na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa JAB, Wakili Patrick Kipangula, wakati akiwasilisha mada kuhusu “Uhuru wa Vyombo vya Habari katika Enzi ya Kidijiti: Wajibu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari” kwenye Kongamano la Uhuru wa Vyombo vya Habari lililoandaliwa na Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) kupitia Idara ya Sanaa na Taaluma za Habari.

Wakili Kipangula amesema maboresho hayo yanalenga kupanua wigo wa wanufaika wa mfumo wa ithibati kwa kuwajumuisha wahitimu wa taaluma hizo mara tu wanapomaliza masomo yao, hatua itakayowawezesha kuwa tayari kuingia katika soko la ajira au kujihusisha na shughuli za kitaaluma zinazohitaji ithibati wakati wowote.

Amesema kwa sasa Kanuni  za Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229, zinamtaka mwombaji wa ithibati kuwasilisha nyaraka za kitaaluma pamoja na barua ya utambulisho kutoka kwa mwajiri au chombo cha habari, taasisi au jukwaa analopeleka kazi zake za kitaaluma.

Kwa mujibu wa Kipangula, mapitio ya kanuni hizo yatawezesha kuondoa changamoto zinazowakabili baadhi ya wahitimu wapya ambao wanakidhi sifa za kitaaluma lakini bado hawajapata waajiri au taasisi za kuwapatia barua za utambulisho zinazohitajika katika mchakato wa maombi ya ithibati.

Awali kabla ya kumkaribisha Wakili Kipangula kutoa wasilisho Mkuu wa Idara ya Sanaa na Taaluma za Habari katika Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), Dkt. Deograsia Ndunguru, ameikaribisha Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) kuendelea kuimarisha ushirikiano na Chuo hicho katika maeneo mbalimbali, ikiwemo maboresho ya mitaala ya uandishi wa habari ili kuendana na mabadiliko ya teknolojia na mahitaji ya sekta ya habari.

Shule ya Royal Family English Medium Primary School imeendelea kujijengea sifa kubwa baada ya kuibuka kinara kwa kushika nafasi ya kwanza katika Manispaa ya Geita kati ya shule 91 katika mtihani wa Moko ya Kanda ya Ziwa.

Shule hiyo yenye wanafunzi 77 wa darasa la saba walioshiriki mtihani huo wameonyesha kiwango cha juu cha ufaulu ambapo wanafunzi 76 wamepata wastani wa A na mwanafunzi mmoja pekee akipata wastani wa B.

Akizungumza baada ya kutangazwa kwa matokeo hayo Mkurugenzi wa shule Mhandisi Lazaro Philipo amesema mafanikio hayo ni matokeo ya ushirikiano mkubwa kati ya walimu, wazazi na wanafunzi.

Ameishukuru jamii kwa kuendelea kuiamini shule hiyo na kuahidi kuongeza juhudi zaidi ili kuifanya Royal Family kuwa kitovu cha elimu bora na maadili mema nchini.


NA MWANDISHI WETU, DODOMA


Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) na Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Taifa (MCC), Mary Chatanda amesema mageuzi makubwa ya kimaendeleo yaliyofanywa na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan yamekuwa chachu ya vyuo vikuu vya ndani na nje ya Tanzania kumtunuku Shahada mbalimbali za Heshima za Uzamivu.

Chatanda ametoa kauli hiyo Juni 5, 2026, Jijini Dodoma ikiwa ni siku moja imepita tangu Chuo Kikuu cha Urafiki wa Watu wa Urusi (RADN University) kumtunuku Shahada ya Udaktari wa Heshima (Honoris Causa), Jijini Moscow, Urusi.

"Unajua utendajikazi mzuri wa Rais wetu Dk. Samia unaonekana duniani kote, na wengi wanaridhishwa na juhudi kubwa zinazofanywa ana serikali katika kuchochea maendeleo ya nchi. Rais amefanya mageuzi makubwa ya kimaendeleo, na ndiyo maana wenzetu wa Urusi wamemtunuku Shahada ya Udaktari wa Heshima," amesema Chatanda.

Sambamba na hilo, Chatanda amesema katika kila sekta, kuna mabadiliko chanya mengi ambayo yamefanyika ndani ya muda mfupi, ndiyo maana hata mataifa mengine yanatambua kazi nzuri zinazofanyika nchini.

Juni 4, 2026, Chuo Kikuu cha RADN kilimtunuku Rais Dk. Samia Shahada ya Udaktari wa Heshima ikiwa ni njia ya kutambua mchango wake katika mageuzi ya sekta ya elimu, kuimarisha hadhi ya Tanzania kimataifa ikiwemo sekta ya utalii.

Baada ya kutunukiwa Shahada hiyo, Rais Dk. Samia amesema mafanikio hayo si yake pekee yake bali ni juhudi za pamoja kama nchi.

"Shahada hii haihusu mafanikio yangu binafsi, bali ni utambuzi wa mchango wa Watanzania wote katika maendeleo ya Taifa na ushirikiano wa kimataifa. Napokea kwa upole, kama Rais wa Tanzania, mtoto wa Afrika na rafiki wa Russia. Siipokei kwa ajili yangu, bali kwa ajili ya Watanzania," amesisitiza Rais Dk. Samia.

Rais Dk. Samia yupo nchini Urusi kwa ziara ya kikazi, ikiwa ni juhudi za kuimarisha diplomasia ya uchumi na mataifa mengine ili kukuza maendeleo endelevu ya kiuchumi na kijamii nchini.


Balozi wa Finland nchini, Bi. Theresa Zitting (kushoto) na Mkurugenzi wa Misitu na Ufugaji wa Nyuki kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii Bw. Daniel Pancras wakizindua rasmi Muongozo wa Uwekezaji katika Sekta ya Misitu Tanzania wakati wa hafla ya Siku ya Misitu ya Finland iliyofanyika Jijini Dar es Salaam.

UBALOZI wa Finland nchini Tanzania, kwa ushirikiano na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) Tanzania kupitia Mpango wa Ubunifu wa FUNGUO, wameadhimisha Siku ya Misitu ya Finland 2026 yenye kaulimbiu “Kufanya Biashara na Finland.”

Tukio hilo limewakutanisha wafanyabiashara, wawekezaji, taasisi za Serikali, wadau wa maendeleo, wajasiriamali, na wataalamu wa misitu kutoka Finland na Tanzania ili kuimarisha ushirikiano wa kibiashara na ukuaji endelevu katika sekta ya misitu.

Mpango huu ulihusisha mada kuu kuhusu fursa za uwekezaji katika sekta ya misitu Tanzania, mawasilisho kutoka kwa makampuni ya Finland, jukwaa maalumu la kukutanisha , na maonyesho ya ufumbuzi endelevu wa misitu kutoka nchi zote mbili.

Hafla hii pia ilishuhudia uzinduzi wa muongozo maalumu wa uwekezaji katika sekta ya misitu (Tanzania Forest Sector Investment Guide).

Akizungumza juu ya umuhimu wa tukio hilo, Balozi wa Finland Tanzania Theresa Zitting amesisitiza umuhimu wa ushirikiano wa kibiashara wa nchi hizi mbili. “Ushirikiano madhubuti wa kibiashara ni muhimu katika kufungua fursa zote za sekta ya misitu Tanzania. Siku ya Misitu ya Finland inatoa fursa ya kipekee kwa makampuni, wabunifu, na wawekezaji kutoka nchi zote mbili kujenga uhusiano, kubadilishana ujuzi, na kubainifursa za kivitendo za ushirikiano,” alisema Balozi Zitting na kuongeza kuwa tukio hili linaashiria dhamira ya muda mrefu ya Finland katika maendeleo endelevu ya kiuchumi ya Tanzania kupitia uwekezaji, ubunifu, na ushirikiano na sekta binafsi.

Akiwakilisha Serikali ya Tanzania Mkurugenzi wa Misitu na Ufugaji wa Nyuki, Wizara ya Maliasili na Utalii, Bw. Daniel Pancras, ameupongeza mpango huu na kusisitiza jinsi unavyoendana na vipaumbele vya maendeleo vya Tanzania. “Sekta ya misitu ya Tanzania ina fursa nyingi kubwa ambazo bado hazijatumiwa kikamilifu, na Finland imekuwa miongoni mwa wabia wetu thabiti na wenye mchango mkubwa katika kufanikishahili. Uhusiano wa namna hii wa kibiashara wa moja kwa moja ndio hasaunaohitajika ilikutafsiri malengo yetu ya pamoja kuwa ajira, kuongeza thamani, na ukuaji endelevu.”

Taasisi ya Finnpartnership imewasilisha huduma zake kwa washiriki wa Tanzania, ikitengeneza fursa mpya za ushirikiano na makampuni ya Finland na upatikanaji wa mifumo ya ufadhili wa pamoja iliyoundwa kusaidia ukuaji wa biashara na ubia wa kimataifa.

Akizungumza kwaniaba ya FinFund, Naibu AfisaMtendaji Mkuu Minnamari Marttila ameangazia fursa za mageuzi zinazotokana na mikutano ya kibiashara iliyoratibiwa vizuri. “Siku ya Misitu ya Finland inatengeneza mazingira, ambapo makampuni yanaweza kwenda mbalizaidi ya utambulisho tu na kuanza kujenga uhusiano wa maana wa kibiashara kupitia kubadilishana ujuzi, uhamishaji wa teknolojia, uwekezaji, na ushirikiano wa mudamrefu wa kibiashara.”

Kivutio kikuu cha siku hii kimekuwa ni maonyesho ya makampuni yanayofadhiliwa kupitia Mpango wa #GreenCatalyst, ambao unaofadhiliwa na Finland chini ya Mradi wa Ubunifu wa FUNGUO unaomilikiwa na UNDP Tanzania. Mpango huu unakamilisha mradi mkubwa zaidi wa Finland unaojulikana kama FORLAND wenye thamani ya Sh61 bilioni za Kitanzania, ukiimarisha zaidi usaidizi wa ukuaji endelevu na jumuishi katika sekta ya misitu Tanzania.

Kupitia awamu yake ya kwanza ya ufadhili, Mpango wa #GreenCatalyst umewekeza zaidi ya Sh1 bilioni za Kitanzania katika makampuni 14 yanayoendeleza misitu endelevu, usindikaji wa mbao unaoongeza thamani, teknolojiazinazohimili mabadiliko ya tabianchi, na ufumbuzi wa uchumi mzunguko.

Uwekezaji huu unajengwa juu ya dhamira ya muda mrefu ya Finland katika sekta ya misitu Tanzania. Ndani ya kipindi cha miakakumi (10), Finland imewekeza €45 milioni (takribani Sh136.3 bilioni za Kitanzania) katika sekta hii, ikisaidia usimamizi endelevu wa misitu, uendelezaji wa ujuzi, ubunifu, na ushirikiano wa sekta binafsi unaochangia ukuaji wa uchumi na uendelevu wa mazingira.

Akizungumza kwa niaba ya UNDP Tanzania, Meneja wa Mradi wa FUNGUO Joseph Manirakiza aliangazia nafasi ya ushirikiano katika kukuza ubunifu. “Ubunifu unastawi pale ambapo wajasiriamali wanapatasiotu ufadhili, bali pia mitandao, masoko, na ushirikiano. Siku ya Misitu ya Finland ni jukwaa la aina yake ambalo wajasiriamali wetu wa #GreenCatalyst wanalihitaji ili kuunganishwa na kukua,” alisema Manirakiza.

Naye mwakililishi wa FORLAND ambao ni mradi unaojihusisha na misitu, matumizi sahihi ya ardhi na kuongeza thamani katika mazao ya misitu, Bw. Masasa Makwassa aliipongeza Finland kw akuadhimisha siku hii muhimu na kusisitiza kuwa shirika hilo litaendelea kushirikiana na wadau wote kuhakikisha malengo ya mradi huo unotekelezwa kwa pamoja na Tanzania na Finland yanafikiwa.

Na. Jordan Mbwambo, WF, Dodoma,

Serikali imefafanua vigezo vinavyotumika katika utozaji wa Kodi ya Majengo (Property Tax) kupitia Mfumo wa Mita za Umeme za LUKU, hatua inayolenga kurahisisha ukusanyaji wa kodi na kuongeza ufanisi katika usimamizi wa mapato ya ndani.

Hayo yameelezwa bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula (Mb), alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Mhe. Tinnar Andrew Chenge, aliyetaka kujua kigezo kinachotumiwa na Serikali katika kutoza Kodi ya Majengo kupitia Mfumo wa Mita za LUKU.

“Kwa sasa Serikali inatumia viwango mfuto katika kutoza kodi ya majengo kupitia mita za umeme za LUKU. Vigezo vinavyotumika kutoza kodi ya majengo kupitia LUKU ni nyumba ya kawaida ambayo inatozwa shilingi 18,000 kwa mwaka au shilingi 1,500 kwa mwezi na nyumba ya ghorofa ambayo inatozwa shilingi 90,000 kwa kila sakafu kwa mwaka au shilingi 7,500 kwa kila sakafu kwa mwezi,” alisema Mhe. Luswetula.

Aidha, alisema kuwa nyumba za nyasi, udongo, majengo ya huduma za jamii, ibada pamoja na nyumba zinazoishi wazee wenye umri wa miaka 60 na kuendelea hazitozwi Kodi ya Majengo isipokuwa pale majengo hayo yanapotumika kwa shughuli za biashara.

Mhe. Luswetula alisema kuwa utaratibu huo unalenga kuhakikisha mfumo wa utozaji kodi unaendelea kuwa rahisi, wenye ufanisi na unaozingatia makundi maalum yanayostahili msamaha kwa mujibu wa sheria.
Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula (Mb), akijibu swali la Mbunge wa Ilemela, Mhe. Tinnar Andrew Chenge, aliyetaka kujua, kigezo kinachotumiwa na Serikali katika kutoza Kodi ya Majengo kupitia Mfumo wa Mita za Luku, bungeni jijini Dodoma.(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Fedha)

Farida Mangube, Morogoro

Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Morogoro imebaini dosari katika mfumo wa ukusanyaji wa mapato na kufanikisha kurejeshwa kwa zaidi ya Shilingi milioni 69 ambazo zilikuwa hazijakusanywa, hatua inayodhihirisha juhudi za taasisi hiyo katika kulinda mapato ya serikali na kuhakikisha fedha za umma zinatumika kwa ufanisi.

Akizungumza na waandishi wa habari kuhusu utekelezaji wa shughuli za TAKUKURU kwa kipindi cha Januari hadi Machi 2026, Naibu Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Morogoro, Christopher Mwakajinga, alisema kiasi cha Shilingi 69,248,392 kilikusanywa baada ya operesheni maalumu ya kufuatilia makusanyo ya mapato kupitia mashine za POS zinazotumia mfumo wa TAUSI. 

Alisema uchunguzi ulibaini kutokuwiana kwa taarifa za makusanyo kati ya mfumo huo na taasisi za kifedha, hali iliyosababisha kuonekana kwa madeni yasiyo halisi kabla ya dosari hizo kurekebishwa.

 Taasisi hiyo pia ilifuatilia utekelezaji wa miradi minane ya maendeleo yenye thamani ya zaidi ya Shilingi bilioni 2.7 kwa lengo la kuhakikisha thamani ya fedha inapatikana. 

Aliongeza kuwa ushauri wa kitaalamu uliotolewa na TAKUKURU uliwezesha kuokolewa au kurejeshwa matumizi yenye thamani ya zaidi ya Shilingi bilioni 15.7 katika sekta mbalimbali ikiwemo elimu, afya na maji.

Kwa upande wa elimu kwa umma, alisema TAKUKURU iliendesha semina 74, mikutano ya hadhara 19 na kuhamasisha uanzishwaji na uimarishaji wa klabu 100 za kupinga rushwa. Aidha, taasisi hiyo ilipokea malalamiko 94 kutoka kwa wananchi, ambapo 65 yalihusu tuhuma za rushwa na kuanza kufanyiwa kazi, huku 29 yakielekezwa kwa mamlaka husika kwa hatua zaidi.

Aliwataka wananchi kuendelea kushirikiana na TAKUKURU kwa kutoa taarifa za vitendo vya rushwa kupitia namba ya bure 113, simu 0738 150 143 au katika ofisi za taasisi hiyo zilizo karibu nao. Baadhi ya wananchi wa Manispaa ya Morogoro wamepongeza juhudi hizo wakisema zimechangia kuokoa fedha za umma na kuimarisha utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwa manufaa ya wananchi.



Na. OWM (KAM) Dodoma

Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Dkt. Evaline Munisi amekutana na kufanya kikao kazi na Wakurugenzi pamoja na wataalamu wa Idara ya Ajira na Ukuzaji Ujuzi kutoka Ofisi hiyo kwa lengo la kuimarisha utekelezaji wa majukumu, kuongeza ufanisi wa kazi na kuimarisha ushirikiano katika utoaji wa huduma kwa wananchi.

Katika kikao hicho kilichofanyika ofisini kwake Dodoma Juni 04,2026 , Dkt. Munisi ameitaka idara hiyo kuongeza juhudi katika kutangaza fursa mbalimbali za ajira na programu za ukuzaji ujuzi zinazotolewa na Serikali ili kuwafikia Watanzania wengi zaidi na kuwawezesha kunufaika na fursa hizo kwa wakati.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa ubunifu, uwajibikaji na ushirikiano katika utekelezaji wa majukumu ya idara hiyo ili kuhakikisha huduma zinazotolewa zinakuwa na tija, zinawafikia walengwa ipasavyo na kuchangia maendeleo ya kiuchumi na kijamii nchini.

 Dkt. Munisi ameelekeza idara hiyo kuweka mkazo katika uboreshaji wa takwimu za soko la ajira na kufanya tathmini ya mara kwa mara ya mahitaji ya ujuzi katika sekta mbalimbali. Alisema hatua hiyo itawezesha Serikali kuandaa programu zinazoendana na mahitaji halisi ya waajiri na soko la ajira kwa ujumla.

Kwa upande wao, Wakurugenzi wa Idara hizo Bi.Alana Nchimbi na Bi.Jane Sorogo wamemshukuru Naibu Waziri kwa maelekezo na mwongozo alioutoa ambapo wameahidi kuongeza kasi ya utekelezaji wa mipango ya idara, ikiwemo kuimarisha ushirikiano na sekta binafsi, vyuo vya ufundi na taasisi za elimu ya juu ili kuhakikisha vijana wanapata ujuzi unaohitajika sokoni.

Kikao hicho ni sehemu ya jitihada endelevu za Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano kuhakikisha kuwa Sera ya Taifa ya Ajira ya mwaka 2008 inatekelezwa kwa vitendo, changamoto za ajira zinapungua na fursa za kiuchumi zinapanuliwa kwa vijana na makundi mengine katika jamii.





Top News