Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira NEMC Leo Februari 9, 2026 limekifunga kiwanda cha urejelezaji wa taka za plastiki cha HOOTA kilichopo Kata ya Vikindu Mkoani Pwani kutokana na kutekeleza shughuli zake kinyume na taratibu za kimazingira.

Akizungumza mara baada ya timu ya wataalamu wa Mazingira kutoka NEMC kukagua kiwanda hicho, Meneja Utekelezaji wa Sheria (NEMC) Mhandisi Luhuvilo Mwamila ameeleza changamoto zilizobainika katika kiwanda hicho ikiwa ni Pamoja kuanzisha kiwanda bila kufanya Tathmini ya Athari kwa Mazingira (TAM) na kutokuwa na cheti cha Mazingira, kuanzisha kiwanda katikati ya makazi ya watu hivyo kuhatarisha usalama wa wakazi wa maeneo hayo, pia kukosa teknolojia madhubuti ya kudhibiti hewa ya kemikali inayosababishwa na uendeshaji wa kiwanda hicho, kukosekana kwa vifaa kinga kwa wafanyakazi na utiririshaji wa maji taka kwenye makazi ya watu bila kuyatibu.

Ameeleza kuwa, awali NEMC ilikagua kiwanda hicho na kutoa maelekezo ambayo kiwanda hicho kinatakiwa kuzingatia lakini hakikutekeleza maagizo hayo hivyo Baraza limechukua hatua ya kukifungia kiwanda hicho mpaka kitakapo tekeleza maelekezo yote yaliyotolewa na NEMC.

Ameongeza kuwa NEMC inaunga mkono uwekezaji nchini kwa kuwataka wawekezaji wote kufuata taratibu zote za Kimazingira zinazotolewa na NEMC zikiwemo kufanya Tathmini ya Athari kwa Mazingira na kupatiwa cheti Cha Mazingira.

Kwa upande wake, Kaimu Meneja wa Kanda ya Mashariki Kusini (NEMC) Bw. Noel Kikwale amezitaka Mamlaka zinazohisika na Mipango miji kutenga Maeneo maalumu ya viwanda na kuhakikisha wawekezaji wanafanya shughuli zao katika Maeneo hayo ili kuepuka changamoto za kimazingira na afya ya wananchi.

Ukaguzi huo ulihusisha wataalamu wa Mazingira kutoka NEMC wakiongozwa na Meneja wa Utekelezaji wa Sheria Mhandisi Bi. Luvilo Mwamila na Viongozi wa Kata ya Vikindu na wa Serikali za mitaa.






Na Mwandishi Wetu,Zanzibar

Waziri wa Kilimo, Umwagiliaji, Maliasili na Mifugo Zanzibar, Mhe. Suleiman Masoud Makame, amelishukuru Wakala wa Kimataifa wa Nguvu za Atomiki Duniani (IAEA) kwa namna shirika hilo linavyoisaidia Zanzibar katika sekta ya kilimo na mifugo.

Akizungumza katika ofisi za Wizara ya Kilimo Zanzibar baada ya kupokea ugeni kutoka IAEA, ugeni ulioongozwa na Bwana Gashaw Gebeyehu Wolde, Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kiufundi kwa Afrika, pamoja na Bi. Azza Kashlan, Afisa wa Usimamizi wa Programu, Waziri Makame alisema wizara yake itaendelea kushirikiana kwa karibu na IAEA ili kuhakikisha ushirikiano huo unaimarika zaidi, kama ambavyo umefanikiwa katika maeneo ya mazao na mifugo.

Kwa upande wake, Bwana Gashaw Gebeyehu Wolde alisema kuwa IAEA ina miradi ya kitaifa nchini Tanzania katika sekta ya kilimo, na nia yao ni kuona miradi hiyo inaleta matokeo chanya kwa wananchi.

Naye Prof. Najat Kassim Mohammed, Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Nguvu za Atomiki Tanzania (TAEC), alieleza kuwa kulikuwa na mradi wa kilimo uliomalizika mwaka jana, na kikao kilichofanyika Zanzibar kitasaidia kufanikisha tafiti mpya zitakazosaidia kupambana na wadudu wanaoshambulia matunda, jambo litakalowaletea wananchi maendeleo ya moja kwa moja.

Ziara hiyo ilionyesha dhamira ya IAEA ya kuendeleza ushirikiano wake na Zanzibar, hususan katika sekta za kilimo na mifugo, ili kuongeza usalama wa chakula, kuboresha maisha ya wananchi, na kuimarisha maendeleo endelevu visiwani.



 

Mwakilishi wa Katibu Tawala wa Mkoa wa Shinyanga Bw. David Lyamongi,akizungumza wakati wa semina ya kuwajengea uelewa kuhusu masuala ya ushindani wa kibiashara wadau na wafanyabiashara wa mkoa wa Shinyanga iliyofanyika  katika Ukumbi wa Makindo, Shinyanga.

Na.Mwandishi Wetu-SHINYANGA

Baraza la Ushindani, kwa niaba ya Mwenyekiti wake, Mhe. Jaji Rose Ally Ebrahimu, limewashukuru wadau na wafanyabiashara wa Mkoa wa Shinyanga kwa kujitokeza kwa wingi kushiriki katika semina ya kuwajengea uwezo iliyofanyika  katika Ukumbi wa Makindo, Shinyanga.

Semina hiyo imelenga kuwaongezea wadau uelewa kuhusu masuala ya ushindani wa kibiashara, haki zao kama wafanyabiashara pamoja na taratibu za kuwasilisha rufaa endapo hawataridhishwa na maamuzi ya mamlaka za udhibiti.

Akifungua semina hiyo, Bw. David Lyamongi, aliyemwakilisha Katibu Tawala wa Mkoa wa Shinyanga, CP Salumu Hamduni, aliwataka wadau na wafanyabiashara kutumia vyema fursa hiyo ya kujifunza ili kuimarisha shughuli zao za kibiashara.

Aidha, aliishukuru Baraza la Ushindani kwa kuwaletea wakazi wa Shinyanga elimu muhimu inayolenga kulinda haki zao katika biashara na kuimarisha ushindani wa haki katika soko.

Akizungumza katika semina hiyo, Msajili wa Baraza la Ushindani, Mhe. Mbegu Kaskasi, alisema kuwa Baraza la Ushindani ni chombo cha Serikali kilichoanzishwa kwa lengo la kusikiliza na kutatua migogoro ya ushindani wa kibiashara. Alisisitiza kuwa Baraza linaendelea kutoa elimu kwa umma ili kuhakikisha wadau na wafanyabiashara wanalifahamu, kulifikia kwa urahisi na kulitumia ipasavyo wanapohitaji haki.

Kwa upande wake Mjasiriamali kutoka Mkoa wa Shinyanga , Bw. Dedani Rutazibwa,alipongeza Baraza la Ushindani kwa kuandaa semina hiyo ya kuwajengea uwezo wadau. Alisema kutokana na umuhimu wa chombo hicho, ameiomba Serikali kupitia Baraza la Ushindani kuendelea kutoa elimu kwa makundi mbalimbali katika ngazi tofauti, ili wafanyabiashara waweze kufahamu haki zao pamoja na mamlaka sahihi za kuwasilisha rufaa zinazotokana na maamuzi ya mamlaka za udhibiti na Tume ya Ushindani.

Naye  Mkazi wa Shinyanga Mwl. Zezema Nyangaki, alisema kuwa elimu aliyopata kupitia semina hiyo imemfungua macho, akieleza kuwa awali hakuwa na uelewa kuhusu uwepo wa mamlaka za udhibiti zinazopokea malalamiko ya wafanyabiashara. Aliongeza kuwa mafunzo hayo yamemsaidia kufahamu kuwa endapo hataridhishwa na maamuzi ya mamlaka hizo, anaweza kukata rufaa katika Baraza la Ushindani ili kupata haki yake kwa mujibu wa sheria.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akiwa na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe. Prof. Adolf Mkenda (kulia) pamoja na Viongozi mbalimbali, wakionesha Mpango wa Ushirikiano kati ya Taasisi za Elimu na Viwanda mara baada ya kuuzindua katika hafla iliyofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) Jijini Dar es Salaam, leo tarehe 09 Februari 2026.



Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akizindua Mpango wa Ushirikiano kati ya Taasisi za Elimu na Viwanda katika hafla iliyofanyika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) Jijini Dar es Salaam, leo tarehe 09 Februari 2026.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akihutubia wakati wa Uzinduzi wa Mpango wa Ushirikiano kati ya Taasisi za Elimu na Viwanda uliyofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) Jijini Dar es Salaam, leo tarehe 09 Februari 2026.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, akiwa na Viongozi mbalimbali katika picha ya pamoja na baadhi ya Waajiri, mara baada ya kuzindua Mpango wa Ushirikiano kati ya Taasisi za Elimu na Viwanda katika hafla iliyofanyika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) Jijini Dar es Salaam, leo tarehe 09 Februari 2026.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akiwasili katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) Jijini Dar es Salaam kwaajili ya Uzinduzi wa Mpango wa Ushirikiano kati ya Taasisi za Elimu na Viwanda, leo tarehe 09 Februari 2026.


Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akiwa na Viongozi mbalimbali wakati akishiriki Uzinduzi wa Mpango wa Ushirikiano kati ya Taasisi za Elimu na Viwanda uliyofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) Jijini Dar es Salaam, leo tarehe 09 Februari 2026.








MKUU wa Jeshi la Polisi nchini IGP Camillus Wambura, amesema Jeshi la Polisi litaendelea kuweka jitihada za kununua mbwa wapya wa kisasa na wenye uwezo ili kuboresha muonekano wa mbwa wa Polisi mwenye umbo lenye kumdhoofisha mhalifu.

IGP Wambura, ameyasema hayo wakati wa Ufunguzi wa Kikao Kazi cha Wakuu wa Kikosi cha Mbwa na farasi wa Mikoa na Wataalam Waongoza Mbwa na Farasi kikao kilichofanyika jijini Dar es salaam Februari 9,2026 huku akiweka msisitizo kwenye eneo la utoaji wa elimu kwa jamii kuhusu umuhimu wa kuwatumia Wanyama kazi katika kudhibiti uhalifu kwenye maeneo yao.

Akizungumza na Watendaji hao IGP Wambura, amebainisha kuwa, Kikosi hicho kina umuhimu mkubwa kiusalama kwa kuwa Doria za mipakani na maeneo mengine muhimu hulazimika kutumia mbwa na farasi kwani ni rahisi kupenya kwenye maeneo ambayo gari haliwezi kupita kwa urahisi.

Amesema, Jeshi la Polisi lina Mbwa na Farasi wanaofanya kazi katika bandari, viwanja vya ndege na mipakani kwa lengo la kuzuia biashara za magendo na usafirishaji haramu wa silaha pamoja na dawa za kulevya, hivyo amewataka kuendelea kuweka nguvu ya kutosha kuhakikisha kuwa, muda wote mipaka yetu inakuwa salama kwa kushirikiana na askari kutoka vikosi vingine ili kudhibiti uhalifu.

Aidha, IGP Wambura, ametoa wito kwa Watendaji wa Kikosi hicho hususani tunapojiandaa na mashindano ya AFCON 2027 ambapo Tanzania ni mojawapo ya nchi Mwenyeji wa Mashindano hayo, kuhakikisha wanakuwa na mbwa na farasi bora wenye mafunzo ya viwango vya kimataifa ili waweze kutoa huduma bora isiyokuwa na mashaka na ambayo itasaidia kuiletea sifa nchi yetu.

Nae Kamishna wa Operesheni na Mafunzo CP Awadhi Juma Haji, amempongeza Mkuu wa Jeshi la Polisi kwa kuendelea kuboresha kikosi cha Mbwa na Farasi na kuhakikisha kikosi kinatekeleza majukumu yake ipasavyo ya kukabiliana na matukio mbalimbali ya kihalifu ikiwemo udhibiti wa dawa za kulevya, silaha haramu pamoja na bidhaa nyingine za magendo.

Kamishna Awadhi amesema kikosi hicho kimeweza kushiriki kwenye operesheni za matukio mbalimbali ikiwemo mikutano ya kitaifa na kimataifa ili kuimarisha amani na utulivu wa kutosha na kudhibiti viashiria vyovyote vya kihalifu.

Kwa upande wake Mkuu wa Kikosi cha Mbwa na Farasi Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Namsemba Mwakatobe, amesema kikao kazi hiki kitawezesha kubadilishana uzoefu na kujengeana uwezo wa kiutendaji hivyo washiriki wa kikao kazi hicho wataenda kuleta mabadiliko ya kiutendaji kwenye maeneo yao kwa kuhakikisha wanadhibiti uhalifu.

Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete akipokea nakala ya kitabu "Jamhuri na Plato" kilichotafsiriwa na Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere kutoka kwa Bw. Walter Bgoya, Mkurugenzi wa kampuni ya uchapishaji ya Mkuki na Nyota, mwishoni mwa juma jijini Dar es Salaam.

Kitabu hiki, asili yake ikiwa ni The Republic (Politeia) cha mwanafalsafa wa Kigiriki Plato, kinajadili mazungumzo ya Socrates, ambapo Plato anachambua aina za tawala, asili ya nafsi, nadharia ya maumbo na dhana ya mji bora (Kallipolis) unaoongozwa na wanafalsafa-wafalme.

Tafsiri hii ya Mwalimu Nyerere inaleta fikra hizi karibu na muktadha wa Afrika, ikisisitiza maadili, uongozi wenye hekima na wajibu wa raia katika kujenga jamii bora.
Dkt Kikwete alikabidhiwa pia nakala ya vitabu vya wasifu na hotuba vya Rais wa Awamu ya Tatu Hayati Benjamin William Mkapa.

Top News