Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Dodoma imeendelea kusogeza huduma zake karibu na wananchi kupitia Ofisi Inayotembea, hatua inayolenga kurahisisha upatikanaji wa huduma za kodi na kuwasaidia walipakodi kutimiza wajibu wao kwa ufanisi.

Akizungumza wakati wa utoaji wa huduma hizo, Meneja wa TRA Mkoa wa Dodoma, Pendolake Elinisafi, amesema Ofisi Inayotembea ni sehemu ya mkakati wa TRA wa kuwafikia wananchi moja kwa moja katika maeneo yao ili kuwapatia huduma mbalimbali za kikodi bila kulazimika kufika katika ofisi za Mamlaka ya Mapato Tanzania.

Ameeleza kuwa huduma zinazotolewa kupitia Ofisi Inayotembea ni pamoja na usajili wa Namba za Utambulisho wa Mlipakodi (TIN), utoaji wa elimu ya kodi, ushauri wa masuala mbalimbali ya kikodi pamoja na utatuzi wa changamoto zinazowakabili walipakodi.

Elinisafi amewahimiza wananchi na wafanyabiashara wa Mkoa wa Dodoma kutumia fursa hiyo kwa kujitokeza kwa wingi ili kupata huduma na maelezo sahihi yatakayowawezesha kutekeleza wajibu wao wa kulipa kodi kwa maendeleo ya taifa.

Makamu Mwenyekiti wa Soko la Wazi la Machinga Complex, Shaban Simba, amesema Ofisi Inayotembea imekuwa na mchango mkubwa katika kurahisisha upatikanaji wa TIN na namba za malipo (Control Number), jambo ambalo limewawezesha wafanyabiashara kulipa tozo za uendeshaji wa soko kwa urahisi na kwa wakati.

Aidha, amesema huduma hiyo imechangia kubadilisha mtazamo wa baadhi ya wafanyabiashara ambao hapo awali walikuwa na uelewa mdogo kuhusu masuala ya kodi, huku ikiwasaidia kufahamu wajibu wao na namna utozaji wa kodi unavyofanyika kwa mujibu wa sheria.

Naye mfanyabiashara wa soko hilo, Tatu Bilimo, amesema kuwa uwepo wa Ofisi Inayotembea umewarahisishia kupata huduma muhimu za kikodi moja kwa moja katika maeneo yao ya biashara, hivyo kuokoa muda na gharama walizokuwa wakitumia kufuata huduma hizo katika ofisi za TRA.

Wafanyabiashara hao wameiomba TRA kuendelea kutoa huduma hiyo, wakieleza kuwa itachochea ushiriki mkubwa zaidi wa wafanyabiashara katika mfumo rasmi wa kodi na kuongeza mchango wao katika kukuza mapato ya Serikali na maendeleo ya taifa kwa ujumla.



Na Mwandishi wetu,Unguja

Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya katika kuongeza jitihada za kuweza kuongeza ufanisi mkubwa katika saula zima la uwajibikaji na kujinza mambo mbali mbali imeamua kwenda kufanya ziara maalumu ya kikazi Zanibar katika visiwa vya eneo la Unguja ambayo itaweza kuwasaidia watendaji pamoja na madiwani katika kuongeza weledi na utekelezaji wa majukumu yao mbali mbali ya kila siku.

Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya Mbeya Bi. Erica Yegella amebainisha kwamba katika ziara hiyo wameambatana na baadhi ya watendaji pamoja na madiwani mbali mbali kwa lengo la kuweza kwenda kujifunza mafunzo mbali mbali kwa kioindi cha siku nne ambayo yataweza kuwasaidia katika suala zima la utekelezaji wa majukumu yao ya kikazi ya kila siku.

Yegella amesema kwamba lengo kubwa la Rais wa awamu ya sita Dkt. Samia Suluhu Hassan ni kuwahudumia wananchi wake na kuleta chachu ya maendeleo na mabadiliko makubwa katika nyanja mbali mbali hivyo ana imani kwamba kufanyika kwa ziara hiyo kwa upande wa madiwani itawezamkuleta tija na mkombozi mkubwa kwa wananchi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya kutokana na mafunzo ambayo watajifunza.

"Nashukuru sana mimi pamoja na baadhi ya waatendaji pamoja na madiwani wangu wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya tumefika salama na tumepokelewa vizuri sana Zanzibar na kwamba tumekuja maalumu kwa ajili ya ziara ya kikazi ya siku nne ambapo tutakuwepo katika maeneo mabali mbali ya Unguja na wenyeji wetu akiwemo Mkurugenzi mtendaji wa mjini magharibi ametupokea kwa heshima zote,"amebainisha Bi. Yegella.

Kadhalika Mkurugenzi huyo amesema katika ziara hiyo wataweza kupata fursa ya kujifunza masuala mbali mbali na kubadilishana uzoefu katika kutekeleza majukumu yao ikiwe pamoja na kutembelea miradi mbali mbali ya maendeeleo kwa ajili ya kujifunza jinsi wanavyoweka mikakati katika kutekeelza miradi hiyo.

Kwa upande wake Mkurugenzi mtendaji wa Manispaa ya mjini Magharibi Bi. Sabra Machano amesema kwamba amefarijika sana na ujio wa ziara hiyo kutoka kwa uongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya na kuahidi kuwapa ushirikiano wa hali na mali katika kipindi chote watakapokuwa katika ziara ya mafunzo hayo.

Naye Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya BI. Aiddah Haule amesema kwamba mafunzo ambayo watayapata wakiwa katika visiwa hivyo vya unguja yeye pamoja na jopo la madiwani pamoja na mkurugenzi wapo yatakuwa ni mkombozi mkubwa katika kuleta mageuzi katika nyanja mbali mbali ikiwa ni pamoja na kuwahudumia wananchi katika maeneo yao mbali mbali.






Na Janeth Raphael MichuziTv .

Serikali imezindua rasmi programu ya Grand Challenges Tanzania, jukwaa jipya la kitaifa litakalolenga kuimarisha utafiti, sayansi, teknolojia na ubunifu kwa lengo la kupata suluhu endelevu za changamoto zinazoikabili jamii katika sekta mbalimbali za maendeleo nchini.

Uzinduzi huo umefanyika jijini Dodoma ambapo Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Wanu Hafidh Ameir, amemwakilisha Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, amesema mpango huo unafungua fursa mpya kwa watafiti, wabunifu na taasisi za Kitanzania kuibua na kuendeleza teknolojia pamoja na tafiti zenye matokeo yatakayoboresha maisha ya wananchi na kuchochea maendeleo ya Taifa.

Aidha, amesema uzinduzi wa programu hiyo unaendana na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayotambua nafasi ya sayansi, teknolojia, utafiti na ubunifu kama nguzo muhimu za maendeleo ya kiuchumi na kijamii. Pia aliipongeza Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH), The Science for Africa Foundation, Taasisi ya Afya ya Ifakara pamoja na washirika wengine wa maendeleo kwa kushirikiana kuanzisha mpango huo.

Kwa upande wa Mkurugenzi Mkuu wa COSTECH, Dkt. Amos Nungu, amesema kila kizazi hukabiliwa na changamoto zake, huku kizazi cha sasa kikikabiliwa na masuala ya usalama wa chakula, afya, ajira kwa vijana, uhifadhi wa mazingira na matumizi ya fursa zinazotokana na mapinduzi ya kidijitali. Alisisitiza kuwa wataalamu, taasisi za utafiti na wabunifu wa Tanzania wanapaswa kuwa mstari wa mbele katika kubuni suluhisho zinazolingana na mazingira na mahitaji ya nchi.

Dkt. Nungu amesema Grand Challenges Tanzania inalenga kuwakutanisha watafiti, wabunifu, watunga sera, sekta binafsi, washirika wa maendeleo na jamii kwa ujumla ili kushirikiana kutafuta majibu ya changamoto zinazowagusa wananchi moja kwa moja. Kwa mujibu wake, mafanikio ya jukwaa hilo yatategemea uwezo wa kubadilisha maarifa yanayotokana na tafiti na ubunifu kuwa matokeo yenye manufaa kwa wananchi.

Amebainisha kuwa Tanzania tayari imeweka msingi imara katika sekta ya sayansi na teknolojia kupitia uwekezaji uliofanyika kwa miaka kadhaa. Zaidi ya shilingi bilioni 129 zimehamasishwa kupitia Mfuko wa Taifa wa Kuendeleza Sayansi na Teknolojia kwa ajili ya kusaidia tafiti, maendeleo ya teknolojia, ubunifu na miundombinu ya kisayansi, huku Serikali ikichangia zaidi ya shilingi bilioni 85. Uwekezaji huo umewezesha kuanzishwa kwa maabara, vituo vya ubunifu na programu za kuwajengea uwezo watafiti pamoja na vijana wabunifu.

Sambamba na uzinduzi huo, COSTECH imetangaza kuwa itazindua Wito wa Kwanza wa Utafiti wa Grand Challenges Tanzania utakaowapa nafasi watafiti na wabunifu kuwasilisha mawazo bunifu yenye uwezo wa kutoa suluhisho kwa changamoto halisi za maendeleo. Kipaumbele kitawekwa kwa miradi inayohusisha ushirikiano wa taaluma mbalimbali pamoja na ushiriki wa vijana watafiti, wabunifu chipukizi, wanawake wanasayansi na taasisi kutoka maeneo mbalimbali ya nchi.

Serikali imeeleza kuwa mafanikio ya Grand Challenges Tanzania yatapimwa kwa kiwango ambacho tafiti na ubunifu vitachangia kuboresha afya, ustawi wa jamii, usalama wa chakula, uhifadhi wa mazingira na ukuaji wa uchumi, huku ikitoa wito kwa wadau wa sekta za umma na binafsi kuendelea kushirikiana kuendeleza ajenda ya sayansi, teknolojia na ubunifu nchini.







Na Mwandishi Wetu, Uswisi

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Deus Sangu ameongoza ujumbe wa Tanzania kushiriki katika Mkutano Mkuu wa 114 wa Shirika la Kazi Duniani (ILO) unaofanyika Jijini Geneva, nchini Uswisi.

Akizungumza leo Juni 4, 2026 Waziri Sangu amesema mkutano huo umekuwa na manufaa makubwa kwa Taifa katika kujadili masuala ya haki za wafanyakazi, kusimamia viwango vya kazi ili kuwa na stahiki kulingana na makubaliano ya pamoja chini ya Shirika la Kazi Duniani.

Amebainisha maeneo makuu ya mjadala katika mkutano huo wa mwaka 2026 ni Masuala mbalimbali yanayohusu Sekta ya Kazi Duniani, Utekelezaji wa mikataba mbalimbali ambayo Tanzania imeridhia chini ya ILO na Matumizi ya Akili Unde (AI) inavyoweza kutumika katika kuhakikisha kazi za staha zinazingatiwa kwa wafanyakazi.

Pia amesema kuwa katika mkutano huo wameweza kujadili na Wadau wa Utatu (Serikali, Waajiri na Wafanyakazi) kutoka Tanzania Bara na Visiwani ili kuona namna bora ya kushirikiana na kuwa na majadiliano ya kijamii ambayo yanaleta tija hususan katika nyakati hizi za matumizi ya teknolojia na ukuaji wa uchumi wa kidijitali.

Wakati huo huo Waziri Sangu amemshukuru Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuruhusu wadau wa utatu kushiriki katika mkutano huo ambao unawawezesha kubadilishana uzoefu na kujadili masuala yanayohusu ustawi wa sekta ya kazi.

Mkutano Mkuu wa 114 wa Shirika la Kazi Duniani (ILO) unaofanyika Jijini Geneva, nchini Uswisi unashirikisha wawakilishi wa Serikali, Waajiri na Wafanyakazi kutoka nchi wanachama 187. Mkutano huo ulianza rasmi tarehe 1 Juni, 2026 na utahitimishwa Juni 12, 2026.




Na Farida Mangube Morogoro

Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kimesisitiza umuhimu wa kuwekeza katika tafiti, ubunifu na teknolojia za uzalishaji wa mbegu bora ili kuongeza tija katika sekta ya kilimo na kuimarisha usalama wa chakula nchini.

Kauli hiyo imetolewa wakati wa mjadala wa masuala ya uwekezaji katika miradi ya maendeleo ya uzalishaji wa mbegu na ubunifu wa teknolojia za kilimo ulioandaliwa na SUA kwa kushirikisha wadau mbalimbali wa sekta ya kilimo, wakiwemo watafiti, taasisi za kifedha, wazalishaji wa mbegu na Taasisi ya Kudhibiti Ubora wa Mbegu Tanzania (TOSCI).

Akizungumza kwa niaba ya Makamu Mkuu wa SUA, Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Taaluma, Utafiti na Ushauri wa Kitaalam Prof. Maulid Mwatawala alisema maendeleo ya sekta ya kilimo yanategemea kwa kiwango kikubwa uwekezaji katika teknolojia rahisi, tafiti na ubunifu unaolenga kutatua changamoto zinazowakabili wakulima.

Alisema matumizi ya teknolojia na mbegu bora yanaweza kuongeza uzalishaji wa mazao, kupunguza gharama za uzalishaji na kuwasaidia wakulima kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi, hivyo kuna haja ya kuendelea kuimarisha ushirikiano kati ya taasisi za utafiti, Serikali na sekta binafsi.

Profesa Mwatawala alieleza kuwa SUA itaendelea kutoa mchango wake katika kuzalisha maarifa, teknolojia na wataalamu watakaosaidia kuendeleza sekta ya kilimo na kuhakikisha matokeo ya tafiti yanawafikia wakulima kwa wakati.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa TOSCI, Bw. Nyasebwa Chimagu, alisema taasisi hiyo imejipanga kuimarisha ukaguzi katika maeneo mbalimbali ya uzalishaji na usambazaji wa mbegu ili kuhakikisha wakulima wanapata mbegu zilizothibitishwa na zenye ubora unaotakiwa.

Alisema uuzaji wa mbegu feki unahatarisha mafanikio ya wakulima na unaweza kusababisha hasara kubwa katika uzalishaji wa mazao, jambo linaloweza kuathiri juhudi za taifa katika kuhakikisha upatikanaji wa chakula cha kutosha.

“Hatutasita kuchukua hatua kali kwa mtu yeyote atakayebainika kukiuka sheria za uzalishaji na uuzaji wa mbegu. Tunataka kulinda maslahi ya wakulima na kuhakikisha wanapata mbegu bora zinazowezesha kuongeza uzalishaji,” alisema Bw. Chimagu.

Nae Mkurugenzi wa Mipango, Ushauri na Mahusiano wa Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB), Bw. Mkani Waziri, alisema kuna umuhimu wa mifumo ya sekta ya kilimo kuunganishwa kidijitali ili kurahisisha upatikanaji wa huduma za kifedha kwa wakulima.

Alisema matumizi ya mifumo ya kidijitali yatawawezesha wakulima kupata mikopo na huduma nyingine za kifedha kwa urahisi zaidi bila kujali mahali walipo, hatua itakayochochea ukuaji wa sekta ya kilimo na kuongeza ushiriki wa wakulima katika uchumi wa kisasa.

Wadau waliohudhuria mjadala huo walikubaliana kuwa uwekezaji katika mbegu bora, teknolojia za kisasa, tafiti za kilimo na huduma za kifedha ni nguzo muhimu katika kuifanya sekta ya kilimo kuwa yenye tija, ushindani na mchango mkubwa katika maendeleo ya uchumi wa nchi.




Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, ametembelea banda la Benki ya NMB katika Tamasha la Uwekezaji Zanzibar 2026 lililofanyika Golden Tulip Airport Hotel, Zanzibar.

NMB ilikuwa miongoni mwa wadhamini wa tamasha hilo la kila mwaka lililowakutanisha viongozi wa serikali, wawekezaji, taasisi za fedha, watendaji wakuu na wadau wa sekta binafsi kujadili fursa za uwekezaji na ukuaji endelevu wa uchumi wa Zanzibar.

Rais Dkt. Mwinyi alipokelewa na Meneja wa Benki ya NMB, Tawi la Zanzibar, Ahmed Nassor, ambaye alimweleza kuhusu suluhisho mbalimbali zinazopatikana kupitia NMB kwa wawekezaji, kampuni na taasisi zinazofanya kazi Zanzibar.

Akizungumza katika banda hilo, Nassor alisema ushiriki wa NMB katika tamasha hilo unaonesha utayari wa benki hiyo kuendelea kuwa mshirika wa karibu wa Serikali na sekta binafsi katika kuchochea ukuaji wa uchumi wa Zanzibar.

“Kwa NMB, Tamasha la Uwekezaji Zanzibar ni jukwaa muhimu la kuonesha suluhisho tulizonazo kwa wawekezaji, makampuni na taasisi zinazofanya kazi Zanzibar. Tupo tayari kusaidia mahitaji yao ya kifedha kupitia huduma za kibenki, malipo, makusanyo na mifumo ya kidijitali, huku tukiendelea kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kusukuma mafanikio makubwa zaidi ya kiuchumi kwa Zanzibar,” alisema Nassor.



















Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) imezindua kampeni maalum inayofahamika kama “Tunakuona Mbali”, ikiwa ni sehemu ya jitihada zake za kuwawezesha Watanzania kutoka makundi mbalimbali ya kijamii kufikia malengo yao ya maendeleo kupitia huduma rasmi za kifedha.

Kampeni hiyo inalenga kuhamasisha utamaduni wa kuweka akiba, kuwekeza, kutumia huduma za kifedha kwa usahihi na kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu fursa zinazotolewa na benki katika kuboresha maisha yao. Kupitia kampeni hiyo, NBC inalenga kuwafikia wafanyakazi, wakulima, watoto, vijana, wanafunzi, wanawake, wastaafu, vikundi vya kijamii, taasisi za dini, Watanzania wanaoishi nje ya nchi pamoja na wafanyabiashara wadogo, wakati, na wakubwa.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa kampeni hiyo uliofanyika katika makao makuu ya benki hiyo jijini Dar es Salaam mapema leo, Mkuu wa Kitengo cha Masoko wa NBC, Bw. David Raymond, alisema kampeni hiyo imejengwa juu ya falsafa ya kutambua na kuunga mkono ndoto na juhudi za Watanzania katika hatua mbalimbali za maisha yao.

“Tunaposema ‘NBC Tunakuona Mbali’, tunamaanisha kuwa tunakupa zaidi ya huduma za kawaida za benki. Tunatambua kwamba kila Mtanzania ana ndoto na malengo ya kufikia mafanikio katika maisha yake; iwe ni kujenga nyumba, kukuza biashara, kusomesha watoto, kuanzisha uwekezaji au kujijengea usalama wa kifedha kwa sasa na siku zijazo. Ndiyo maana, kama taasisi ya kifedha, tunajiona kuwa mshirika wa safari hiyo ya maendeleo.

Akaunti ya NBC ni zaidi ya mahali pa kuhifadhi fedha; ni suluhisho kamili la kifedha mfano wa ‘wallet’ inayokuwezesha kufanya miamala ya kila siku kwa urahisi,ni mahali pa kuweka akiba, kutuma na kupokea pesa, kupata mikopo, kuwekeza katika masoko ya hisa na mifuko ya uwekezaji, pamoja na kuendesha biashara yako kwa ufanisi zaidi. Kupitia huduma hizi, tunalenga kukupa nyenzo na fursa zinazokusaidia kufikia malengo yako na kutimiza ndoto zako,” alisema.

Aliongeza kuwa maendeleo ya mtu mmoja mmoja yana mchango mkubwa katika ukuaji wa uchumi wa taifa. Hivyo, kuwasaidia wananchi kupata elimu sahihi ya fedha, kuweka akiba, kuwekeza na kutumia huduma rasmi za mikopo ni njia muhimu ya kujenga uchumi jumuishi unaowanufaisha wengi zaidi.

“Kila tunapomsaidia mfanyabiashara kukuza mtaji wake, mkulima kuongeza uzalishaji, mzazi kuandaa mustakabali wa mtoto wake au kijana kuanza safari yake ya kifedha, tunakuwa pia tunachangia ukuaji wa uchumi wa nchi. Hiyo ndiyo maana halisi ya kuwaona Watanzania wakifika mbali,” alisisitiza.

Kupitia kampeni hiyo, NBC itatoa elimu ya kifedha na kuhamasisha matumizi ya bidhaa na huduma zake mbalimbali zilizobuniwa kulingana na mahitaji ya makundi tofauti ya kijamii. Miongoni mwa huduma hizo ni Akaunti ya Chanua kwa watoto, Akaunti ya Malengo, Akaunti ya Johari kwa wanawake, Akaunti ya Mwalimu, Akaunti ya Mshahara, Akaunti ya Wajasiriamali, Akaunti ya Waalimu, Akaunti ya Wanafunzi, Akaunti ya Kua Nasi, Akaunti ya Vikundi, Akaunti Binafsi, Akaunti ya Diaspora pamoja na Akaunti za Biashara pamoja na akaunti ya Muda Maalum kwa ajili ya uwekezaji.

Kwa upande wake, Meneja wa Bidhaa na Mauzo wa NBC, Bi. Dorothea Mabonye, alisema kampeni hiyo pia itatoa elimu kuhusu usimamizi wa fedha, matumizi sahihi ya mikopo, huduma za bima, mifumo ya malipo na miamala ya kidigitali ili kuwajengea wananchi uwezo wa kufanya maamuzi bora ya kifedha.

“Kupitia kampeni hii tunataka kuwasaidia Watanzania kutambua kuwa huduma za kifedha si kwa ajili ya kutunza fedha pekee, bali ni nyenzo muhimu ya kufikia malengo yao ya maisha. Tunataka kuona wananchi wakitumia huduma hizi kujenga msingi imara wa maendeleo yao na ya familia zao,” alisema.

Alifafanua kuwa huduma mbalimbali zinazotolewa na benki hiyo zimebuniwa ili kukidhi mahitaji ya kila kundi. “Kwa mfano, wazazi wanaweza kuwawekea watoto wao msingi wa utamaduni wa kuweka akiba kupitia Akaunti ya Chanua huku wafanyakazi pia wakiweza kupata mkopo wa muda mfupi unaowasaidia kukidhi mahitaji ya dharura wanaposubiri muda wa kupokea mshahara’’ alisema

Aliongeza kuwa kupitia akaunti ya Diaspora Watanzania waishio nje ya nchi wanaweza kupata fursa rahisi za kuwekeza na kushiriki maendeleo ya nchi kupitia mikopo ya nyumba na akaunti ya muda maalum ya uwekezaji.

Naye Mkuu wa Huduma za Kidigitali wa NBC, Bw. Ulrik Peter, alisema teknolojia imeendelea kuwa daraja muhimu la kuwafikishia wananchi huduma za kifedha kwa haraka, kwa gharama nafuu na bila vikwazo vya umbali.

Alisema NBC imeendelea kuwekeza katika mifumo ya kidigitali kama vile NBC Kiganjani, NBC Connect, huduma za kadi za benki na mawakala ili kuhakikisha wananchi wengi zaidi wanapata huduma za kifedha bila kulazimika kutembelea matawi ya benki.

“Ujumuishaji wa kifedha hauwezi kufikiwa bila matumizi makubwa ya teknolojia. Kupitia kampeni hii tunawahamasisha wananchi kutumia huduma za kidigitali ambazo zinawawezesha kuokoa muda, kupunguza gharama za miamala na kupata huduma za kifedha popote walipo, wakati wowote na kwa namna wanayohitaji kufanya matumizi yao ya kila siku,” alisema.

Aliongeza kuwa uwekezaji uliofanywa na NBC katika mifumo ya kidigitali na utoaji wa kadi papo hapo kwa wateja wanaofungua akaunti mpya ni sehemu ya mkakati wa kuondoa vikwazo vinavyoweza kuwazuia wananchi kushiriki kikamilifu katika uchumi rasmi na kukua kiuchumi.



Maofisa mbalimbali wa Benki ya NBC wakiongozwa na Mkuu wa Bidhaa na Mauzo, Bw. Abel Kaseko (kushoto) wakipeperusha bendera kuashiria uzinduzi wa kampeni maalum inayofahamika kama “Tunakuona Mbali”, ikiwa ni sehemu ya jitihada za benki hiyo kuwawezesha Watanzania kutoka makundi mbalimbali ya kijamii kufikia malengo yao ya maendeleo kupitia huduma rasmi za kifedha. Hafla ya uzinduzi wa kampeni hiyo imefanyika leo jijini Dar es Salaam.

Na Janeth Raphael MichuziTv - Bungeni Dodoma

Spika wa Bunge, Mussa Azan Zungu, ametoa onyo dhidi ya tabia ya utoro miongoni mwa baadhi ya wabunge na viongozi wa Serikali, akisema hali hiyo imezidi na kuanza kudhoofisha nidhamu pamoja na ufanisi wa shughuli za Bunge.

Akizungumza leo Bungeni jijini Dodoma, Spika Zungu amesema baadhi ya wabunge wamekuwa wakifika asubuhi kusaini mahudhurio kisha kuondoka, na baadaye kurejea jioni kwa ajili ya kusaini tena bila kushiriki vikao vya Bunge.

Amesema pia kuna wabunge wanaosaini mahudhurio kwa niaba ya wenzao ambao hawapo kabisa Bungeni, jambo alilolitaja kuwa ni ukiukwaji wa taratibu za Bunge unaostahili kuchukuliwa hatua za kisheria na kinidhamu.

“Kuna wanaokuja asubuhi, wanasaini na kuondoka. Jioni wanarudi kusaini tena. Wapo pia wanaowasainia wenzao ambao hawapo. Tunawafahamu wanaosaini na wanaosainiwa, na hatua za kibunge zinapaswa kuchukuliwa,” alisema Spika Zungu.

Aidha, amesema kuna kundi lingine la wabunge ambao hawaonekani kabisa katika shughuli za Bunge licha ya kutokuwa na sababu za msingi za kutokuwepo, hali aliyoeleza kuwa ni kudharau mamlaka ya Spika pamoja na wananchi waliowachagua.

Spika Zungu amesisitiza kuwa kuanzia Jumatatu ijayo hatarajii kuona tabia hizo zikiendelea, akibainisha kuwa Ofisi ya Katibu wa Bunge ina uwezo wa kufuatilia na kubaini mahali alipo kila mbunge wakati wa shughuli za Bunge.

Pia aliiagiza Wizara inayosimamia mawasiliano kushirikiana katika kuimarisha mifumo ya ufuatiliaji wa mahudhurio ya wabunge ili kudhibiti utoro huo.

Katika hatua nyingine, Spika alimwelekeza Waziri Palamagamba Kabudi kulifanyia kazi suala hilo kwa kuwa liko chini ya usimamizi wa ofisi yake.

Vilevile, alikemea utaratibu wa baadhi ya mawaziri na manaibu wao kuwa safarini kwa wakati mmoja, akisema hali hiyo husababisha kukosekana kwa uwakilishi wa Serikali ndani ya Bunge.

“Haipendezi Waziri kuwa kwenye ziara huku Naibu Waziri naye akiwa kwenye ziara wakati huohuo. Wapeane zamu ili mmoja awepo Bungeni wakati mwingine akiwa kwenye majukumu ya nje,” alisisitiza.

Kauli ya Spika imekuja wakati Bunge likiendelea na shughuli zake jijini Dodoma, huku akitaka nidhamu ya mahudhurio irejee na kila kiongozi kutimiza wajibu wake kwa wananchi.



Na Mwandishi Wetu, Dodoma
MKURUGENZI Mtendaji wa Kituo cha Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP Centre), David Kafulila, amesema mfumo wa ubia kati ya sekta ya umma na sekta binafsi (PPP) una mchango mkubwa katika kuongeza ufanisi wa taasisi za umma na kuchochea ukuaji wa uchumi wa taifa.

Kafulila alitoa kauli hiyo jana wakati akizungumza katika mhadhara wa umma uliofanyika katika Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), akieleza kuwa mataifa mengi duniani yameendelea kuwekeza katika mfumo wa PPP kutokana na manufaa yake katika kuimarisha utendaji wa taasisi na kuongeza tija ya kiuchumi.

Alisema sababu kuu tatu zinazochochea matumizi ya mfumo huo duniani ni kuvutia mitaji ya sekta binafsi katika utekelezaji wa miradi ya umma, kuongeza ufanisi wa taasisi za serikali na kukuza ubunifu.

“PPP siyo tu njia ya kupata fedha za kutekeleza miradi ya maendeleo, bali ni nyenzo muhimu ya kuongeza ufanisi wa taasisi za umma na kuhamasisha ubunifu unaochangia maendeleo endelevu ya uchumi,” alisema Kafulila.

Alibainisha kuwa tafiti mbalimbali zinaonesha kuwa katika baadhi ya nchi zilizoendelea, takribani asilimia 25 ya utajiri wa taifa unatokana na ufanisi wa taasisi zake, huku rasilimali za asili zikichangia karibu asilimia tano pekee.

Kwa mujibu wa Kafulila, mafanikio ya nchi hizo hayatokani na ukosefu wa rasilimali za asili, bali uwezo wa kujenga mifumo madhubuti inayowezesha matumizi bora ya rasilimali zilizopo.

Alitolea mfano nchi za China, Marekani na Urusi ambazo pamoja na kuwa na utajiri mkubwa wa rasilimali za asili, zimejikita zaidi katika kuimarisha rasilimali watu, ubunifu na taasisi zenye ufanisi mkubwa.

“China inazalisha dhahabu nyingi kuliko nchi yoyote Afrika, Marekani ina mafuta mengi kuliko mataifa mengi duniani na Urusi ina gesi nyingi kuliko nchi yoyote Afrika. Hata hivyo, msingi wa maendeleo yao ni nguvu ya taasisi, ubunifu na rasilimali watu,” alisema.

Kafulila alisisitiza kuwa Tanzania inaweza kunufaika zaidi na mfumo wa PPP kwa kutumia sekta binafsi kama mshirika wa maendeleo katika utekelezaji wa miradi mikubwa ya kimkakati, huku ikiimarisha ufanisi wa taasisi za umma na kuongeza kasi ya ukuaji wa uchumi.






Na Mwandishi Wetu, Mbeya
Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya limeendelea kushirikiana na wananchi na wadau mbalimbali katika kuimarisha ulinzi na usalama wa maisha na mali kupitia doria, misako na oparesheni za kuzuia na kubaini uhalifu. Katika kipindi cha mwezi Mei 2026, jumla ya watuhumiwa 871 wa makosa mbalimbali ya jinai walikamatwa katika maeneo tofauti ya mkoa huo.

Kwa mujibu wa taarifa ya Jeshi la Polisi, makosa yaliyohusika ni pamoja na mauaji, kujeruhi, ubakaji, kupatikana na silaha bila kibali, dawa za kulevya pamoja na wizi. Watuhumiwa waliokamilishiwa upelelezi walifikishwa mahakamani, ambapo baadhi yao wamekutikana na hatia na kuhukumiwa vifungo mbalimbali kwa mujibu wa sheria.

Katika matukio ya hivi karibuni, Polisi wanawashikilia watuhumiwa wawili, Baraka Mwakatobe (31) na Said Baraka (39) wakazi wa Dodoma, kwa tuhuma za kusafirisha vipodozi vyenye viambata sumu vilivyopigwa marufuku nchini. Watuhumiwa hao walikamatwa Mei 28, 2026 katika kizuizi cha Polisi Chimala wakiwa na shehena ya boksi 403 za vipodozi hivyo pamoja na bidhaa nyingine zisizo rasmi.

Aidha, Jeshi hilo linamshikilia Shaban Safari (48) mkazi wa Kyela kwa tuhuma za kupatikana na dawa za kulevya aina ya heroin kete 27 pamoja na bangi. Inadaiwa mtuhumiwa huyo alikamatwa akiwa na dawa hizo zilizofichwa kwenye mfuko wa khaki, huku akituhumiwa kuwa muuzaji wa dawa hizo katika eneo hilo.

Kwa kipindi hicho hicho cha Mei 2026, Polisi wamesema pia waliwakamata watuhumiwa 20 wakiwa na bangi kilo 12.24, watuhumiwa wawili wakiwa na gongo lita 30 na wengine wawili wakiwa na silaha aina ya gobole, hatua inayoonesha kuendelea kudhibiti uhalifu na vitendo vya kihalifu mkoani humo. Aidha, kesi 224 zilifikishwa mahakamani ambapo 122 zilimalizika kwa hukumu za hatia na 73 bado zinaendelea.

Jeshi la Polisi limehimiza wananchi kuendelea kushirikiana kwa kutoa taarifa za uhalifu na kufika mahakamani kutoa ushahidi ili kusaidia haki kutendeka. Pia limetoa onyo kwa watu wanaojihusisha na vitendo vya uhalifu kuacha mara moja, likisisitiza kuwa uhalifu haulipi na hatua kali za kisheria zitachukuliwa kwa wote watakaobainika.

HATIMAE wamesikia na Kukata kiu ya wapenzi watazamaji wa Filamu za kinaijeria ndivyo unaweza sema,Enzi za Ini edo ,aki na ukwa na wengine waliotikisa miaka ya nyuma kwa filamu za kutisha na kufundisha sasa utawaona ndani ya St Swahili.

Meneja Masoko wa Kampuni ya Startimes Limited David Malisa ameweka wazi kuwa kwa Mara ya Kwanza wapenzi wa Filamu za Kinaijeria kwa Watanzania watashuhudia filamu hizo ambazo zimewekewa sauti za kutafsiri kwa Lugha ya Kiswahili kuanzia Jumamosi mpaka Jumapili kuanzia Mwezi Juni mwaka huu.

Akiongeza zaidi kupitia Kampeni yao mpya "Tumejiamulia kukupa Raha" ikiwa na Lengo la kuwaweka karibu watazamaji wa King'amuzi hicho na kuwakaribisha wateja wao wapya kushuhudia maudhui mapya ya kiburudani zaidi kwa ofa kedekede kuanzia kushuka kwa bei ya vifurushi mpaka kununua King'amuzi chenyewe.

Hata hivyo amesema Filamu za Kibongo hazijaachwa nyuma hivyo ni bandika bandua na wanatarajia kuweka ingizo jipya la filamu za kibongo kama sehemu ya Kuendelea kuwapa sapoti Watayarishaji wa Kibongo kupitia chaneli ya St Swahili.




Na Mwandishi Wetu, Arusha
MKURUGENZI wa Mauzo wa Turaco Collection Tanzania, Florenso Kirambata, amesema kuwa maonesho ya Karibu-KiliFAIR 2026 ni jukwaa muhimu la kuitangaza Tanzania kimataifa, kubadilishana uzoefu na kujenga ushirikiano wa kibiashara katika sekta ya utalii inayokua kwa kasi duniani.

Akizungumza wakati akiwasilisha hoteli za Turaco Collection katika maonesho hayo yanayofanyika jijini Arusha, Florenso alisema tukio hilo linawakutanisha wadau mbalimbali wa sekta ya utalii, ukarimu, safari na uwekezaji kutoka Tanzania na mataifa mengine duniani.

Maonesho ya Karibu-KiliFAIR 2026 yanafanyika kuanzia Juni 4 hadi 7, 2026 katika Viwanja vya Magereza, Arusha.

Florenso alisema Turaco Collection imeendelea kuimarisha uwepo wake nchini kupitia hoteli zake katika maeneo mbalimbali. Dar es Salaam kuna Element by Westin Dar es Salaam na Delta Hotels by Marriott Dar es Salaam, huku Kaskazini mwa Tanzania kukiwa na Turaco Ngorongoro Valley Lodge, Tribute Portfolio na Turaco Manyara View Lodge, Tribute Portfolio. Zanzibar, kampuni inamiliki Turaco Nungwi Resort, Tribute Portfolio, Turaco Spice Tree Stone Town, Tribute Portfolio pamoja na Beyt Al Salaam by Turaco.

Alieleza kuwa hoteli zote za Turaco Collection zinazobeba chapa za kimataifa zinaendeshwa kwa kuzingatia viwango vya Marriott International, jambo linalochangia kuimarisha ubora wa huduma, matumizi ya teknolojia za kisasa na utoaji wa uzoefu wa kiwango cha kimataifa kwa wageni wanaotembelea Tanzania.

Akizungumzia matumizi ya Akili Bandia (AI) katika sekta ya ukarimu, Florenso alisema Marriott International inaamini teknolojia hiyo inapaswa kuboresha uzoefu wa wageni kwa kuufanya kuwa wa kibinafsi zaidi, wenye ufanisi mkubwa na rahisi, huku ikidumisha misingi ya ukarimu unaozingatia mahusiano ya kibinadamu.

Alisema kampuni hiyo inaendelea kuwekeza katika teknolojia za AI ili kuboresha mifumo ya uwekaji nafasi za malazi, shughuli za uendeshaji wa hoteli, programu za uaminifu kwa wateja na huduma mbalimbali za wageni.

“Teknolojia haitachukua nafasi ya ukarimu wa kibinadamu, bali itaongeza uwezo wa wafanyakazi wetu kutoa huduma bora zaidi. Mwelekeo wa Marriott International ni kutumia AI kuifanya safari ya mgeni, kuanzia kupanga safari, kuweka nafasi, kuwasili hotelini hadi kuondoka, kuwa rahisi, ya haraka na yenye uzoefu wa kipekee,” alisema Florenso.

Aliongeza kuwa kupitia ushirikiano wake na Marriott International, Turaco Collection inaendelea kufuatilia kwa karibu maendeleo ya teknolojia katika sekta ya ukarimu ili kuhakikisha wageni wanaotembelea Tanzania wanapata huduma zinazokidhi viwango vya kisasa vya kimataifa.









Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Denis Londo, ametembelea banda la Tume ya Ushindani Tanzania (FCC) katika Maonesho ya Kimataifa ya Mbeya City Expo 2026 yanayoendelea katika viwanja vya Uhindini, jijini Mbeya, ambapo alipata fursa ya kujionea shughuli mbalimbali zinazotekelezwa na taasisi hiyo katika kulinda maslahi ya walaji na kuimarisha ushindani wa biashara nchini.

Katika maonesho hayo, FCC imekuwa ikitoa elimu kwa wananchi kuhusu haki za mlaji, namna ya kutambua na kuepuka bidhaa bandia pamoja na umuhimu wa ushindani wa haki katika shughuli za biashara.

Elimu hiyo imevutia mamia ya wananchi waliojitokeza kutembelea banda hilo na kupata ufafanuzi wa masuala mbalimbali yanayohusu biashara, ushindani na ulinzi wa walaji.

Akizungumza wakati akifunga Maonesho hayo yaliyodumu kwa siku tisa Mei 30, 2026 jijini Mbeya, Naibu Waziri Londo alisisitiza umuhimu wa kuendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu madhara ya bidhaa bandia, akieleza kuwa bidhaa hizo zinaathiri afya za watumiaji, kudhoofisha biashara halali na kupunguza mapato ya Serikali.

Kwa upande wake, Mkuu wa Kanda wa FCC - Nyanda za Juu Kusini Bw. Dickson Mbanga, amesema taasisi hiyo imejipanga kuendelea kuimarisha kampeni za utoaji elimu kwa wananchi ili kuwajengea uwezo wa kutambua bidhaa halisi na kuepuka kununua au kutumia bidhaa zisizo na viwango vinavyotakiwa.

Mbanga alisema Maonesho ya Mbeya City Expo yamekuwa jukwaa muhimu la kuifikia jamii kwa karibu na kutoa elimu inayolenga kuongeza uelewa kuhusu sheria za ushindani na hatua zinazochukuliwa dhidi ya wafanyabiashara wanaojihusisha na usambazaji wa bidhaa bandia.

“Tunatumia maonesho haya kuwafikia wananchi wengi zaidi na kuwaelimisha kuhusu hatari za bidhaa bandia na kumlinda mlaji. Lengo letu ni kuhakikisha watumiaji wanakuwa na taarifa sahihi zitakazowasaidia kufanya maamuzi bora wanaponunua bidhaa mbalimbali sokoni,” alisema Mbanga.

Aliongeza kuwa FCC itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali wa biashara na vyombo vya usalama katika kudhibiti bidhaa bandia zinazoingia sokoni, huku ikiendelea kuhamasisha wananchi kutoa taarifa wanapobaini uwepo wa bidhaa zinazotiliwa shaka.

Maonesho ya Mbeya City Expo 2026 yamewakutanisha wadau kutoka sekta mbalimbali za uchumi, biashara na uwekezaji, huku yakitoa fursa kwa taasisi za umma na binafsi kuonesha huduma, bidhaa na mafanikio yao kwa wananchi. Kupitia ushiriki wake, FCC imeendelea kuonesha dhamira ya Serikali ya kulinda walaji na kujenga mazingira ya biashara yenye ushindani wa haki kwa


Top News