Mrajis na Mtendaji Mkuu wa Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania (TCDC) Dkt. Benson Ndiege kushirikiana na Uongozi wa TCDC Sports Club wanunua vifaa vya michezo kwa wachezaji 42 kuelekea mashindano ya Michezo ya Meimosi mjini Njombe.

Vifaa hivyo vimekabidhiwa leo Aprili 14, 2026 jijini Dodoma wakati wa kuwaaga wanamichezo wakielekea mjini Njombe.

Vifaa vilivyonunuliwa ni jezi za mprira wa miguu, viatu, mipira na vifaa vingine vya michezo.



Kamati ya siasa ya Chama cha Mapinduzi ya (CCM) wilayani Kahama mkoani Shinyanga, imepongeza kasi ya Ujenzi wa Barabara ya Kahama-Kakola yenye urefu wa Kilomita 73 Inayojengwa kwa kiwango cha lami kwa Ufadhili Migodi ya Barrick nchini ya Bulyanhulu na North Mara itakayogharimu kiasi cha shilingi bilioni 101.2.Ujenzi wa barabara hii unatekelezwa kampuni ya China Civil Engineering Construction Corporation.


Ujumbe wa kamati ya siasa wilaya ya Kahama ukiongozwa na Mwenyekiti wa CCM wilaya ya Kahama Thomas Myonga ulitembelea mradi huo wa ujenzi wa barabara na kutoa pongezi kwa kampuni ya Barrick nchini yenye ubia na Serikali ya Tanzania kupitia kampuni ya Twiga Minerals kwa kufanya uwekezaji unaoenda sambmba na kufanikisha miradi mikubwa endelevu inayobadilisha maisha ya wananchi kuwa bora ma itakayoacha alama ya kudumu hata kwa vizazi vijavyo.
Thomas Myonga


Akiongea wakati wa ziara hiyo Mwenyekiti wa CCM wilaya ya Kahama Thomas Myonga amesema wamefurahishwa kuona mradi huu mkubwa unaendelea vizuri na mkandarasi yupo kazini na kutoa rai rai kwa mkandarasi kuongeza kasi ya ujenzi ili kuhakikisha mradi huu anakamilisha kwa wakati kama mkataba unavyoelekeza na wananchi waondokane na kero waliyokuwa nayo ya ubovu wa barabara hii kwa muda mrefu.


Alisema ujenzi wa barabara hii ambao umefikia asilimia zaidi ya asilimia 70 ya utekelezaji wake ukikamilika utasaidia kukuza Uchumi wa wananchi wa Mikoa ya Shinyanga na Geita “CCM katika Ilani yake ya Uchanguzi ya Mwaka 2025/30 inayosimamiwa na Serikali ya Rais Dkt Samia Suluhu Hassan iliahidi kutekeleza ujenzi wa barabara hiyo hivyo mkandarasi anapaswa kuhakikisha inakamilika katika muda uliopangwa.
Mhandisi John Kalando


Awali akitoa taarifa ya maendeleo ya Ujenzi , Mhandisi John Kalando kutoka Wakala wa Barabara (TANROADS) amesema tayari Kampuni ya Barrick nchini imeshalipa fedha zote kwa mkandarasi hivyo watahakikisha wanamsimamia ili ikamilike ndani ya muda.


Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Msalala, Mabula Magangila, amesema kamilika kwa barabara hiyo kutasaidia kuondoa adha ya vumbi kwa wakazi wa mji ya Segese, Lunguya na Kakola kutokana na barabara ya awali iliyokuwa na vumbi na kuwa katika hali mbaya ya kutopitika hali iliyokuwa ikiwasababishia hasara kubwa wasafirishaji na kuleta kero kubwa kwa wananchi.


Kutekelezwa kwa mradi huu mkubwa kwa mafanikio ni kielelezo kinachodhihirisha ubia wa Barrick na Twiga unavyofanikisha kuchochea utengenezaji endelevu wa thamani katika uchumi wa Tanzania na jinsi Serikali ikishirikiana na sekta binafsi inavyoweza kuleta matokeo chanya kwa kufanikisha miradi mikubwa endelevu ya kunufaisha wnanchi kwa kipindi cha muda mrefu.











Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) imefanikiwa kukamata boti ya mwendokasi iliyokuwa ikisafirisha dawa za kulevya aina ya mirungi kutoka Mombasa, Kenya kupitia Bagamoyo, mkoani Pwani.

Operesheni hiyo iliyofanyika usiku wa kuamkia Aprili 14, 2026 katika ufukwe wa Magambani, eneo la Kaole Ufundi, ilifanikisha kukamatwa kwa viroba 18 vyenye jumla ya paketi 1,062 za mirungi. Katika tukio hilo, watuhumiwa wanne walikamatwa.

Akizungumza na waandishi wa habari Bagamoyo mkoani Pwani, Kamishna Jenerali wa DCEA, Aretas Lyimo, amewataja waliokamatwa kuwa ni Jamal Ally Faki (35) Shari Omary Salim (28), wote wakazi wa Tanga, Sebastian Protas Shirima (28) mkazi wa Temeke na James Michael Kimaro (27) mkazi wa Buza Dar es Salaam.

“Boti hii imekuwa ikitumika kwa muda mrefu kusafirisha mirungi kwa njia ya bahari kutoka Mombasa kuja Dar es Salaam na tumekuwa tukiifuatilia kwa muda mrefu, taarifa tuliyoitoa hivi karibuni tulieleza kwamba, mirungi imekamatwa kwa wingi kuliko dawa nyingine za kulevya, boti hii ndiyo iliyokuwa inaleta dawa hizo nchini. Na baada ya kuikamata tutakuwa tumedhoofisha mtandao wa usafirishaji wa dawa za kulevya hapa nchini” amesema Kamishna Lyimo.

Alieleza kuwa, mabadiliko ya mbinu za usafirishaji yamejitokeza kufuatia kuimarika kwa operesheni dhidi ya dawa nyingine hatari kama heroin, cocaine, methamphetamine na skanka, pamoja na operesheni za kuteketeza mirungi Same, hali ambayo imesababisha wahalifu kuhamia kwenye mirungi inayosafirishwa kutoka Kenya.

Aidha, amesema Mamlaka inaendelea na operesheni endelevu za kudhibiti uzalishaji na usambazaji wa dawa za kulevya ikiwa ni pamoja na kuteketeza mashamba ya bangi na kufuatilia mitandao mipya ya usafirishaji, huku akitoa wito kwa wananchi kushirikiana kwa karibu na Mamlaka kwa kutoa taarifa zitakazosaidia kukomesha biashara hiyo haramu.

“Serikali iko makini kuhakikisha inadhibiti kabisa uingiaji wa dawa za kulevya nchini, na tutachukua hatua kali dhidi ya yeyote anayejihusisha na biashara hii,” alisema

Kwa upande wake balozi wa shina namba moja katika kitongoji cha Kaole Ufundi, Dominic Masika ameipongeza Serikali kwa hatua nzuri walizochukua katika kukabiliana na dawa za kulevya.

“Tukio hili lililotokea hapa Kaole, Magambani linaonesha nia ya dhati ya Serikali katika kulinda usalama wa wananchi. Naiomba serikali iendelee kufanya operesheni kama hizi, kufanya doria za mara kwa mara na kuwekeza katika maeneo kama haya yenye vichaka kwani yanaweza kutumika vibaya kama sehemu za kupitisha dawa za kulevya,” alisisitiza.

Akizungumzia chanzo cha changamoto hiyo, alieleza kuwa baadhi ya vijana wanajiingiza katika vitendo hivyo kutokana na kukosa uelewa sahihi, licha ya malezi na miongozo wanayoipata kutoka kwa wazazi. Hivyo, amesisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya wazazi, serikali na viongozi wa mitaa katika kupambana na tatizo la dawa za kulevya.








Aprili 13,2026, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Kombo, alikutana na kuzungumza na wanafunzi wa Kitanzania wanaosoma nchini Mauritius katika Chuo Kikuu cha Middlesex na kuwashauri wanafunzi hao kuhusu maisha yao ya masomo pamoja na wajibu wao wa kuiwakilisha Tanzania wakiwa ugenini.

Katika mazungumzo hayo, Waziri Kombo, ambaye aliambatana na Balozi wa Tanzania nchini Mauritius mwenye makazi yake Harare, Zimbabwe, aliwahimiza wanafunzi hao kuwa mabalozi wazuri wa nchi yao na kuzingatia maadili mema ya Kitanzania, nidhamu, na mwenendo unaoendana na heshima ya taifa.

Alisisitiza umuhimu wa kuitangaza Tanzania vyema popote walipo na kuepuka kuwaangusha wazazi wao waliowezesha safari yao ya elimu na kueleza kuwa juhudi zao zinapaswa kuonekana si tu kitaaluma bali pia kitabia.

“Ninyi ni mabalozi wa taifa lenu, hivyo muiwakilishe vyema nchi yenu na msiwaangushe wazazi wenu.

Nimezungumza na Mkuu wa Chuo, amenihakikishia kuwa wanafunzi wa Tanzania mnafanya vizuri na hamna changamoto za kinidhamu,” alisisitiza Balozi Kombo.

Aliwahamasisha wanafunzi hao kutumia mitandao ya kijamii kwa njia chanya ili kupata taarifa sahihi na kunufaika na fursa mbalimbali zinazotolewa na serikali kama za ajira, ufadhili wa masomo na mafunzo yatakayowasaidia kukuza taaluma zao na kujijengea uwezo wa kiuchumi.

Waziri Kombo pia alitahadharisha dhidi ya majaribu yanayoweza kuwapotosha vijana wakiwa nje ya nchi na kuwasihi kuepuka matumizi ya dawa za kulevya, akieleza kuwa baadhi ya vijana hujikuta wakiharibu mustakabali wao kutokana na tamaa ya kujaribu mambo yasiyofaa.

“Msijaribu kila kitu, kuweni na maadili mema na epukeni matumizi ya dawa za kulevya ili muwe vijana bora na viongozi wa kesho,” alionya.

Ziara hiyo ilifanyika sambamba na ushiriki wa Waziri Kombo katika Mkutano wa Tisa wa Bahari ya Hindi uliofanyika Aprili 10 hadi 12 jijini Port Louis, uliowakutanisha Mawaziri wa Mambo ya Nje kutoka nchi 30 zinazozunguka Bahari ya Hindi kujadili fursa, changamoto na maendeleo ya ukanda huo.




















Top News