KAMPUNI ya Taifa Gas imetangaza kuwa haitapandisha bei ya gesi ya majumbani (LPG) licha ya kupanda kwa bei ya bidhaa hiyo kwa takribani asilimia 43 katika soko la kimataifa, hatua inayolenga kulinda watumiaji dhidi ya athari za mabadiliko ya kiuchumi duniani.

Taarifa hiyo iliyotolewa leo Aprili 3, 2026 jijini Dar es Salaam imeeleza kuwa ongezeko hilo la bei duniani limechangiwa na kupanda kwa gharama katika minyororo ya ugavi na usambazaji wa gesi ya kupikia katika wiki za hivi karibuni.

Akizungumza kupitia taarifa hiyo, Meneja Mkuu wa kampuni hiyo, Devis Deogratius, amesema licha ya changamoto hizo, kampuni imeamua kubeba gharama hizo ili kuhakikisha wateja wanaendelea kupata huduma kwa bei nafuu.

“Katika mazingira haya ya sasa, tunayo dhamira ya dhati ya kuwasaidia wateja wetu kwa kubeba athari za ongezeko la gharama ya nishati ya kupikia kwa kutokuongeza bei huku tukihakikisha upatikanaji endelevu wa gesi safi na ya kuaminika,” amesema Deogratius.

Amesisitiza kuwa uamuzi huo unalenga kusaidia shughuli za kiuchumi, hasa kwa kaya na biashara ndogo ndogo zinazotegemea gesi ya kupikia kama chanzo kikuu cha nishati.

Deogratius amebainisha kuwa Taifa Gas inaelewa umuhimu wa nishati hiyo kwa Watanzania wengi, hivyo itaendelea kuhakikisha inapatikana kwa bei nafuu bila kuathiri usambazaji wake.

Aidha, kampuni hiyo imehakikishia umma kuwa itaendelea kusambaza gesi yake kwa uhakika kupitia mtandao wake wa maghala 25 yaliyosambaa nchini, hatua inayolenga kufikia wateja wa mijini na vijijini.

"Uwekezaji uliofanywa katika miundombinu ya usambazaji unaiwezesha kampuni hii kuhudumia maeneo mbalimbali ya nchi kwa ufanisi zaidi na kuendelea kuunga mkono ajenda ya kitaifa na kimataifa ya nishati safi.

Aidha amesema wataendelea kufuatilia mwenendo wa soko la kimataifa na kufanya maamuzi yatakayolinda maslahi ya wateja huku ikidumisha ubora wa huduma zake.
Wito umetolewa kwa wawekezaji na wazalishaji nchini kutumia huduma za Shirika la Viwango Tanzania (TBS), hususan katika sekta ya vipimo (metrolojia), kutokana na kutambulika kwake kimataifa.

Akizungumza na wanahabari Aprili, 2, 2026 jijini Dar-es-Salaam, Afisa Mkuu wa Metrolojia Joseph Kadenge kutoka Shirika la Viwango Tanzania (TBS) amesema kuwa Metrolojia (Sayansi ya Vipimo) ni Moja ya Misingi minne ya Ubora inayoangalia ubora wa vipimo katika mashine zinazotumika katika uzalishaji.

Amesema ubora wa bidhaa unaanzia kwenye mashine zinazozalishia, kama mashine hazina vipimo sahihi basi hata ubora wa bidhaa uko mashakani.

Kadenge ameongeza kuwa TBS ina Maabara ya Taifa (National Metrology Laboratory) ya Vipimo inayotambulika kimataifa kupitia Shirika la Vipimo Duniani (BIPM), huku uwezo wake wa upimaji ukiwa umeorodheshwa katika kanzidata ya kimataifa.

Aidha, maabara hizo zimepata ithibati ya umahiri kutoka taasisi ya kuangalia umahili ya nchi za SADC inayoitwa SADCAS, hatua inayothibitisha ubora wa huduma zake na kuwahakikishia wawekezaji kuwa huduma za vipimo zinapatikana kwa viwango vinavyokubalika kimataifa.

Kupitia umahiri huo, Kadenge ametoa wito kwa wawekezaji na wazalishaji kutokuwa na hofu ya kuwekeza Tanzania kwani upatikanaji wa huduma ya Ugezi (Calibration) zinapatikana kwa urahisi.





Na Karama Kenyunko Michuzi Tv

WAZIRI wa Afya, Mohamed Mchengerwa, amesema Serikali inaendelea kuchukua hatua madhubuti za kuboresha upatikanaji wa dawa na bidhaa za afya katika vituo vyote vya kutolea huduma nchini, huku akisisitiza umuhimu wa kuimarisha mifumo ya ugavi ili kuhakikisha dawa zinapatikana kwa wakati na kwa ubora unaokidhi viwango.

Amesema hayo Aprili 2, 2026 jijini Dar es Salaam wakati wa kikao kazi na wadau wa sekta ya afya kilichofanyika katika Bohari ya Dawa (MSD), Keko, ambapo alibainisha kuwa uwekezaji mkubwa unaofanywa na Serikali umeendelea kuimarisha hali ya upatikanaji wa dawa na kufikia viwango vinavyoridhisha.

“Serikali imeendelea kuboresha mifumo ya usimamizi na ugavi ili kuhakikisha dawa zinafika kwa wakati katika maeneo yote ya nchi. Maboresho haya yanachangia kupunguza changamoto ya upungufu wa dawa katika vituo vya afya,” amesema Mchengerwa.

Aidha, amesema Serikali imeelekeza juhudi katika kuhakikisha kunakuwepo uwiano sahihi kati ya mahitaji halisi na upatikanaji wa dawa, hatua inayosaidia kuongeza ufanisi na matumizi bora ya rasilimali zilizopo.

Katika kikao hicho, Mchengerwa alisisitiza pia umuhimu wa Bohari ya Dawa (MSD) kuendelea kuimarisha mifumo ya usimamizi, manunuzi na usambazaji wa dawa ili kuepuka upungufu katika vituo vya kutolea huduma.

Kwa upande wake, Mganga Mkuu wa Serikali, Grace Magembe, amesema Serikali itaendelea kusimamia matumizi sahihi ya dawa pamoja na kuhakikisha upatikanaji wake katika ngazi zote za huduma za afya nchini.

Dkt. Magembe alisisitiza kuwa dawa si bidhaa ya kawaida bali ni kemikali yenye uwezo wa kutibu au kusababisha madhara iwapo haitatumika kwa usahihi, hivyo usambazaji wake lazima uzingatie uwepo wa wataalamu wenye ujuzi pamoja na miundombinu ya kumhudumia mgonjwa endapo atapata madhara.

Akijibu hoja za wananchi, alisema Serikali inatambua changamoto zilizopo, ikiwemo upatikanaji wa baadhi ya dawa katika zahanati na vituo vya afya, na kwamba hatua zinaendelea kuchukuliwa ili kuboresha hali hiyo.

Kuhusu upatikanaji wa dawa katika ngazi mbalimbali, alisema upangaji wake unazingatia tafiti za kisayansi na Orodha ya Dawa Muhimu (Essential Drug List), ambapo kila ngazi hupangiwa dawa kulingana na aina ya huduma na uwezo wa kituo husika.

Akizungumzia suala la dawa kuisha muda wake (expiries), Dkt. Magembe alisema hali hiyo ni ya kawaida duniani kote kutokana na muda wa matumizi wa dawa na mabadiliko ya kisayansi, na kusisitiza kuwa Serikali haiwezi kuruhusu matumizi ya dawa zisizo na ufanisi.

Alibainisha kuwa kiwango cha dawa zinazoisha muda wake nchini ni asilimia 1.2, chini ya kiwango kinachokubalika kimataifa cha asilimia tano, jambo linaloonesha usimamizi mzuri.

Aidha, alisema Serikali imeanza kushusha huduma za magonjwa adimu kama sickle cell hadi ngazi ya hospitali za wilaya na kuingiza dawa zake katika mfumo wa ununuzi ili kupunguza gharama kwa wananchi.

Dkt. Magembe pia aligusia matumizi ya majina ya dawa (brand names badala ya generic names), akisema Serikali itatoa maelekezo kurekebisha hali hiyo ili kuongeza ufanisi katika upatikanaji wa dawa.

Aliongeza kuwa Serikali imeongeza bajeti ya dawa kutoka takribani shilingi bilioni 30 hadi kufikia bilioni 398 mwaka 2025, hatua iliyosaidia kuongeza upatikanaji wa dawa hadi asilimia 88 kwa sasa.

“Tutajipanga zaidi kutoa elimu kwa wananchi waelewe sayansi ya dawa na matumizi yake, kwa sababu dawa si chakula; ni sumu isipotumika vizuri,” amesema Dkt. Magembe.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Seif Shekalaghe, amesema zaidi ya asilimia 60 ya wagonjwa wanaokwenda hospitali hupatiwa dawa, huku wengine wakipewa ushauri wa mabadiliko ya mtindo wa maisha ikiwemo mazoezi.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa Bohari ya Dawa (MSD), Mavere Tukai, amesema taasisi hiyo imeendelea kuboresha utendaji wake kwa kuimarisha mifumo ya kidijitali, kuongeza ufanisi katika manunuzi na kusogeza huduma karibu zaidi na wananchi.

Ameeleza kuwa ununuzi wa bidhaa za afya kutoka kwa wazalishaji wa ndani umeongezeka kutoka shilingi bilioni 15.9 mwaka 2021/2022 hadi bilioni 98 mwaka 2024/2025, huku lengo la mwaka huu likiwa kufikia kati ya bilioni 120 hadi 130.

Aidha, amesema utegemezi kwa wasambazaji wa nje umepungua kutoka asilimia 82 hadi asilimia 38, wakati ununuzi kutoka kwa wazalishaji wa ndani umeongezeka hadi asilimia 75.

Alibainisha kuwa hatua hizo zimewezesha hata dawa ambazo awali zilikuwa ngumu kupatikana, ikiwemo za saratani, kupatikana kwa urahisi zaidi na kwa gharama nafuu.

Kikao hicho ni sehemu ya jitihada za Serikali za kuendelea kuimarisha sekta ya afya na kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora nchini.

Waziri wa Afya Mohamed Mchengerwa akizungumza na Wananchi mubashara kupitia mfumo ongea na Waziri kupitia namba ya 199, leo Aprili 2, 2026, wakati wa kikao kazi na wadau wa Afya kilichofanyika Bohari ya Dawa, jijini Dar es Salaam








Na Mwandishi Wetu Dar es Salaam

Waziri wa Viwanda naii  Biashara, Judith Kapinga, ameielekeza Tume ya Ushindani (FCC) kuendelea kutoa elimu kwa walaji ili kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kuimarisha ushindani wa soko nchini.
Waziri Kapinga alitoa kauli hiyo wakati wa kilele cha kufunga maadhimisho ya Siku ya Mlaji Duniani, yaliyofanyika katika Hoteli ya Johari Rotana jijini Dar es Salaam.

Amesema kuwa walaji wanapaswa kulindwa kwa kuhakikisha wanapata bidhaa na huduma zilizo bora, salama na zenye viwango vinavyokubalika katika ushindani wa soko.

“Ni muhimu kwa FCC kuendelea kusimamia haki za walaji kwa kuhakikisha wanapata bidhaa bora na huduma zinazokidhi viwango vinavyotakiwa, sambamba na kujenga mazingira ya ushindani wa haki sokoni,” amesema Waziri Kapinga.
Aidha, ameitaka FCC kuendelea kukutana na wadau mbalimbali, wakiwemo wazalishaji na wafanyabiashara, kwa lengo la kusikiliza changamoto zao na kuzitafutia ufumbuzi unaolenga kuboresha mazingira ya biashara na ulinzi wa mlaji.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, Khadija Ngasongwa, amesema maadhimisho ya mwaka huu yamekuwa fursa muhimu ya kuwakutanisha wadau mbalimbali na kuwapatia elimu kuhusu haki za mlaji katika kujenga ushindani imara sokoni.

Amesema FCC itaendelea kulinda soko kwa kuhakikisha mlaji anapata huduma na bidhaa bora zinazokidhi viwango vinavyohitajika.


“FCC itaendelea kuwa nguzo muhimu katika kusimamia haki za walaji pamoja na kuimarisha ushindani wa soko kwa manufaa ya wananchi na uchumi wa taifa,” amesema Ngasongwa.

Aidha, ameongeza kuwa tume hiyo itaendelea kuwa daraja kati ya wazalishaji, wafanyabiashara pamoja na walaji kwa lengo la kuhakikisha utoaji wa huduma na bidhaa bora unazingatiwa wakati wote.


Naye Mwenyekiti wa Baraza la FCC, Aggrey Mulimuka, amesema baraza hilo litaendelea kutoa ushauri wa kitaalamu kwa lengo la kulinda ushindani wa soko unaozingatia maslahi ya mlaji.
Dkt. Mulimuka amesema dhamira ya baraza ni kuhakikisha kuwa ushindani wa soko unakuwa chachu ya upatikanaji wa huduma bora, bidhaa zenye ubora na mazingira rafiki kwa walaji.


Baraza litaendelea na ikiendelea  ushirikiano kati ya Serikali, sekta binafsi na wadau wengine katika kujenga soko lenye ushindani wa haki na manufaa kwa taifa 

Maadhimisho hayo yamebeba Kauli Mbiu ya Bidhaa Salama,Imani kwa mlaji ikiwa  ni  kuimarisha uelewa wa walaji juu ya haki zao.
Waziri wa Viwanda na Biashara Judith Kapinga akizungumza wakati akifunga Kilele cha  Maadhimisho Siku ya Mlaji yaliyoratibiwa na Tume ya Ushindani (FCC) jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Viwanda na Biashara Judith Kapinga akizundua namba ya maalumu ya mawasiliano kwa wateja kuwasiliana na FCC   wakati akifunga Kilele cha  Maadhimisho Siku ya Mlaji jijini Dar es Salaam.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindani (FCC) Khadija Ngasongwa akitoa maelezo kuhusiana na maadhimisho ya siku ya mlaji hadi kufikia kilele chake  yaliyofanyika ,jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Viwanda na Biashara Judith Kapinga akipokea zawadi kutoka kwa Mwenyekiti wa Baraza la FCC Dkt Aggrey Mulimuka wakati  wa Kilele cha  Maadhimisho ya Siku ya Mlaji jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Viwanda na Biashara Judith Kapinga akizungumza wakati akifunga Kilele cha  Maadhimisho Siku ya Mlaji yaliyoratibiwa na Tume ya Ushindani (FCC) jijini Dar es Salaam.

 

Na Saidi Saidi WMJJWM - Dodoma

Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe.Dkt. Dorothy Gwajima, ametoa wito kwa jamii na wazazi kushiriki kikamilifu katika malezi na ulinzi wa watoto, ili kuzuia ongezeko la watoto wanaoishi na kufanya kazi mitaani.

Akizungumza na waandishi wa habari Aprili 01, 2026 jijini Dodoma kuelekea Maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Mtoto anayeishi na kufanya kazi mtaani, yatakayofanyika Aprili 12, 2026 Jijini Dar Es Salaam yakiwa na Kaulimbiu isemayo “Malezi na Ulinzi wa Mtoto, Wajibu wetu Sote”.

Amesema ushiriki wa pamoja ni muhimu ili kuhakikisha watoto wanakua katika mazingira salama na yenye maadili mema huku akisisitiza jukumu la malezi si la wazazi pekee, bali ni la jamii nzima.

Aidha, Waziri Gwajima ameeleza kuwa changamoto kama umasikini, migogoro ya kifamilia, na ukatili dhidi ya watoto zimekuwa zikichangia watoto wengi kukimbilia mitaani.

Ameibainisha pia mafanikio ya juhudi za Serikali katika kuwaokoa watoto wa mitaani kuwa zaidi ya watoto 5,000 wameunganishwa na familia zao tangu kuanza kwa kampeni ya kuwaokoa watoto wa mitaani mwaka 2025.

Vilevile, Serikali imeanzisha mifumo mbalimbali, ikiwemo madawati ya ustawi wa jamii katika vituo vya usafiri na makao ya watoto, ili kuhakikisha watoto waliookolewa wanapata huduma muhimu kama elimu, afya, na malezi bora.

Waziri Gwajima ametoa wito kwa Watanzania kushirikiana na Serikali kwa kutoa taarifa za ukatili dhidi ya watoto na kuhakikisha wanapata malezi bora. Amesisitiza kuwa watoto wa mitaani wanapaswa kulindwa na kupewa fursa sawa za maendeleo, akihitimisha kwa kusema kuwa ni jukumu la kila mmoja kuhakikisha hakuna mtoto anayelazimika kuishi au kufanya kazi mitaani.

Waziri Gwajima ametumia nafasi hiyo pia kuwashukuru wadau wote wanaoshirikiana na Serikali katika kuhakikisha malezi ya watoto yanaimarishwa hususani shirika SoS Village na Railway Children.

Akizungumza kwa niaba ya mkuu wa mkoa wa Dodoma, mkuu wa wilaya ya Dodoma Jabir Shekimweri, amesisitiza umuhimu wa ushirikiano wa wadau wote katika kukabiliana na changamoto ya watoto wanaoishi na kufanya kazi mitaani, akieleza hatua mbalimbali zilizofikiwa na mkoa wa Dodoma.

Shekimweri amesema mwaka 2024 hadi 2026 Serikali ya mkoa imewaunganisha watoto 293 na familia zao.






NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

Madereva wa viongozi mashuhuri (VIP) wa Jeshi la Polisi wametakiwa kuweka mbele jukumu lao la msingi la kulinda maisha ya viongozi wanaowaendesha kwa kuzingatia tahadhari na kuzuia ajali zinazoweza kuepukika, ili kulinda rasilimali watu muhimu kwa taifa.

Wito huo umetolewa na Mkuu wa Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT), Dkt. Prosper Mgaya, wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya mwezi mmoja kwa madereva wa viongozi hao yanayofanyika chuoni hapo.

Dkt. Mgaya amesema madereva wa VIP wanapaswa kufanya kazi kwa weledi, umakini na nidhamu ya hali ya juu, akisisitiza kuwa viongozi wa juu huandaliwa kwa muda mrefu kwa ajili ya kulitumikia taifa, hivyo kupoteza maisha yao kutokana na uzembe wa madereva ni hasara kubwa kwa nchi.

Aidha, amewahimiza washiriki wa mafunzo hayo kuyachukulia kwa uzito ili yawaletee mabadiliko chanya na kuwasaidia kupanda madaraja kutoka ngazi za chini hadi za juu.

Kwa upande wake, Mkuu wa Usafirishaji Makao Makuu ya Jeshi la Polisi, SACP Fortunatus Muslim, amesema mafunzo hayo yanalenga kuwajengea madereva ujuzi wa kisasa ili kuendana na mabadiliko ya teknolojia ya magari yanayotumiwa na viongozi wa juu, jambo litakalosaidia kuongeza usalama barabarani.

Naye Mkuu wa Chuo cha Taaluma ya Polisi Dar es Salaam na Mratibu wa Mafunzo hayo, DCP Dkt. Lazaro Mambosasa, amewataka madereva kuzingatia viapo vyao vya kazi na kuepuka tabia zisizofaa wanapokuwa kazini.

Ametoa mfano wa baadhi ya vitendo visivyokubalika, ikiwemo madereva kudodondeshea gari upande alipokaa kiongozi wakati wa ajali na kisha kutoweka eneo la tukio, akisisitiza kuwa nidhamu ni msingi wa kazi hiyo.

Ameongeza kuwa madereva watakaoshindwa kufuzu mafunzo hayo hawatatunukiwa vyeti wala kupandishwa madaraja.

Pia amesisitiza kuwa jukumu la dereva halikomei kumfikisha kiongozi anakoenda pekee, bali linahusisha kujilinda yeye mwenyewe, kuwalinda watumiaji wengine wa barabara pamoja na kulinda magari ya viongozi yanayogharimu fedha nyingi za walipa kodi.









Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imeweka rekodi mpya kwa kukusanya shilingi trilioni 3.58 katika mwezi wa Machi 2026 pekee, ikiwa ni sawa na ufanisi wa asilimia 107.6 ya lengo lililowekwa.

Mafanikio hayo yameiwezesha TRA kukamilisha robo ya tatu ya mwaka wa fedha (Januari hadi Machi 2026) kwa kukusanya jumla ya shilingi trilioni 9.31, ikiwa ni ongezeko la asilimia 23.6 ikilinganishwa na kipindi kama hicho mwaka uliopita.

Ufanisi huo umetokana na maboresho makubwa ya mifumo ya TEHAMA, hususan kuanza kutumika kwa mfumo mpya jumuishi wa kodi za ndani (IDRAS) mwezi Februari 2026, uliowezesha kusajili walipakodi wapya zaidi ya 69,000 pamoja na kuunganishwa kwa taasisi 92.

Aidha, kuimarika kwa mfumo wa forodha wa TANCIS kumechangia kuharakisha uondoshaji wa mizigo na kudhibiti mianya ya upotevu wa mapato katika vituo vyote vya forodha nchini.

Kamishna Mkuu wa TRA, Bw. Yusuph Juma Mwenda, amesema mafanikio hayo yanatokana na utekelezaji wa maelekezo ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhimiza ulipaji kodi wa hiari kupitia ujenzi wa mahusiano mazuri kati ya TRA na walipakodi.


Wakala ya Barabara Tanzania (TANROADS) umebaini kuwepo kwa watu wanaojihusisha na vitendo vya utapeli kwa kujifanya watumishi wa wakala, maeneo mbalimbali hususani katika mkoa wa Dodoma.

Kwa mujibu wa taarifa kwa umma iliyotolewa na Mtendaji Mkuu wa TANROADS mapema wiki hii, imeelezwa kuwa taarifa zilizopokelewa zinaonyesha matapeli hao wamekuwa wakiwasiliana kwa njia ya simu na wamiliki wa mabango ya matangazo (billboards), nakujitambulisha kama maafisa wa TANROADS na kudai malipo ili kuzuia kuondolewa kwa mabango yaliyokwisha muda wake.

Taarifa hiyo imeongeza kuwa mbinu zinazotumika na matapeli hao ni pamoja na kutumia lugha ya mamlaka, kutoa vitisho vya kuchukua hatua za kisheria, na kuwaharakisha walengwa kufanya malipo ili kuepuka hatua hizo. Hali hii imekuwa ikiwalenga zaidi wafanyabiashara na wamiliki wa mabango ambao mikataba yao imefikia ukomo.

Kutokana na udanganyifu huo, baadhi ya wananchi tayari wameathirika kwa kupoteza fedha zao baada ya kutuma malipo kwa namba binafsi walizopewa na matapeli hao. TANROADS imesisitiza kuwa haitoi huduma kwa kupokea malipo kupitia namba binafsi za simu au kwa mtu mmoja mmoja, Badala yake, malipo yote hufanyika kupitia mifumo rasmi ya serikali inayotambulika.

Wananchi wametahadharishwa kuwa makini, kuthibitisha taarifa kabla ya kufanya malipo yoyote, na kuepuka kabisa kutuma fedha kwa mtu yeyote anayewasiliana kwa njia hiyo na kujitambulisha kama mtumishi wa TANROADS bila kufuata taratibu rasmi.

Ameeleza kuwa, TANROADS inaendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi kufuatilia utapeli huo ili kuwabaini wahusika na kuchukua hatua kali za kisheria dhidi yao

Wananchi wote wamehimizwa kutoa taarifa za matukio ya aina hiyo kupitia ofisi za TANROADS zilizo karibu au kwa kutumia njia rasmi za mawasiliano za wakala huo, Ushirikiano wa wananchi unatajwa kuwa muhimu katika kusaidia kukomesha vitendo hivyo vya uhalifu.

TANROADS imeeleza kuwa itaendelea kuchukua hatua madhubuti kulinda maslahi ya wananchi na kuhakikisha huduma zake zinatolewa kwa uwazi, usalama na uadilifu, huku ikiwataka wananchi kuwa sehemu ya mapambano dhidi ya matapeli kwa kutoa taarifa mapema wanapobaini viashiria vya udanganyifu.



WIZARA ya Kilimo imesema mafanikio katika kilimo cha mpunga nchini yametokana na uwekezaji wa kimkakati wa Serikali, huku ikiielekeza COPRA kuimarisha usimamizi wa masoko ili kuongeza tija.

Akizungumza katika ufunguzi wa Mkutano wa Kitaifa wa Wadau wa Zao la Mpunga uliofanyika Machi 30, 2026 mkoani Morogoro, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo anayesimamia Maendeleo ya Mazao na Usalama wa Chakula, Prof. Peter L. M. Msofe, alisema sekta hiyo imepata mageuzi makubwa.

Alisema uzalishaji wa mchele umefikia tani milioni 2.6 katika mwaka 2024/2025, ukilinganishwa na mahitaji ya tani milioni 1.2, hali iliyoifanya Tanzania kuwa na ziada ya tani milioni 1.4.

Prof. Msofe aliongeza kuwa ziada hiyo imewezesha kuuza nje tani 298,715 za mchele katika masoko ya EAC na SADC na kuingiza zaidi ya shilingi bilioni 333.5 za fedha za kigeni.

Pamoja na mafanikio hayo, alibainisha kuwa bado kuna fursa ya kuongeza tija zaidi, akieleza kuwa wastani wa uzalishaji ni tani 3.2 kwa hekta dhidi ya uwezo wa kufikia tani 6 kwa hekta.

Aidha, alisema Serikali inalenga kuongeza uzalishaji hadi tani milioni 8 ifikapo 2030 na kupunguza upotevu wa mazao baada ya mavuno kutoka asilimia 25 hadi chini ya asilimia 10.

Kwa upande wa COPRA, Bi. Pendo Biganmbo, Mkurugenzi wa Idara ya Maendeleo ya Mazao na Viwango, aliyemwakilisha Mkurugenzi Mkuu, alisema wameanza usajili na utoaji wa leseni kwa wafanyabiashara wa mpunga ili kuimarisha usimamizi wa soko.

Alisema zoezi hilo litahusisha pia wakulima kusajiliwa pamoja na mashamba yao ili kuongeza ufanisi katika mnyororo mzima wa thamani wa zao la mpunga.
Shirika la Utafiti na Maendeleo ya Viwanda Tanzania (TIRDO) imewaalika wadau wa ngozi nchini kupata mafunzo juu ya uchakataji na utengenezaji bidhaa za ngozi nchini .

Hayo yameelezwa na Kaimu Mkurugenzi wa TIRDO Mhandisi Ramson Mwilangali wakati akifunga mafunzo ya siku tano kwa wanafunzi na wazalishaji wa Bidhaa za ngozi nchini .

Mafunzo hayo ya siku tano yamelenga kuwajengea uwezo wazalishaji wa ngozi kutoka mikoa ya Pwani , Morogoro,Dar es salaam na Kilimanjaro lengo likiwa ni kuhakikisha ngozi inayozalishwa hapa nchini inachakatwa na kuzalisha bidhaa tofauti na sasa ambapo kwa kiasi kikubwa ngozi inauzwa nje ya nchi kabla ya kuchakatwa .

Mhandisi Ramso amesema kuwa soko la Tanzania inahitaji zaidi ya jozi ya viatu milioni 54 huku Viwanda vya ndani vikizalisha jozi elfu tatu tu ambayo ni chini ya asilimia kumi ya mahitaji bidhaa hiyo kwa mwaka.

"Tunalenga kuongeza uzalishaji wa ndani kufikia asilimia 50 ya mahitaji ya nchi ili kuziba pengo linaloagizwa kutoka nje .

Kwa upande wa mtaalam ngozi wa na nguo kutoka TIRDO Mhandisi Yusufu Sampuli amesema kuwa lengo lilikuwa ni kutoka mafunzo kwa watu 15 lakini kutokana na uhitaji wamefika watu 28 kutoka mikoa hiyo mitano . "Tumepokea wanufaika wa mafunzo haya waliopo katika hatua mbali mbali ,wengine wamewahi kuzalisha viatu ,wengine ni mara yao ya kwanza lakini Kila Mmoja ametoka hapa na utaalam wa kutosha juu ya hatua za uzalishaji na utambuzi wa ubora wa ngozi aliongeza Mhandisi Sampuli.

Mafunzo hayo yametoleaa kwa wazalishaji wa bidhaa kama viatu, mabegi ,mikanda nk kwa wamiliki wa viwanda vidogo pamoja na wajasiriamali wadogo na wakubwa juu ya elimu ya uboreshaji bidhaa za ngozi.

Baadhi ya wanufaika wa mafunzo hayo Bi.Yusra Omary Ally Kutoka Dar es salaam , Ndugu Piscus Maresh kutoka Pwani na Bi Pauline Kawa wameshukuru Kwa mafunzo hayo na kuishukuru TIRDO Kwa kuwapa nafasi ya kujifunza.

Mmoja wa washiriki hao Bi Yusra Omary amesema kuwa ni mara yake ya kwanza kupata mafunzo hayo lakini ndani ya siku nne ameweza kutengeneza kiatu kwa hatua ya kwanza ya kupima ngozi, kukata hadi kukamilika kabisa. "Mimi siku zote nilikuwa na wazo lakini sikujua nianzie wapi ,kupitia mafunzo haya Sasa naweza kutengeneza kiatu katika hatua zote aliongeza Bi Yusra.

Mafunzo hayo yamedhaminiwa na Wizara ya Viwanda na Biashara , Jumuhia ya Umoja wa Ulaya ,Jumuhia ya Afrika Mashariki pamoja na kituo Cha Biashara cha Kimataifa (ITC ) chini ya mradi wake wa MARKUP II inayolenga kusaidia uzalishaji wa Bidhaa Bora za ngozi barani Afrika .

Wataalam kutoka TIRDO walioshiriki katika kufanikisha mafunzo hayo kwa vitendo Mhandisi Yusufu Sampuli, Kenan Tarimo , Paul Kimathi pamoja na Innocent Barongo ambao kwa pamoja wametoa wito kwa wanufaika hao wa mafunzo kutosita kuwasiliana nao pamoja na kufika TIRDO kupata ushauri wa kitaalam pamoja na upimaji wa Kimaabara.











Top News