Na Pamela Mollel,Arusha 

Katibu Tawala wa Mkoa wa Arusha, Dk. Toba Alnason Nguvila, ameweka mkazo katika kuimarisha sekta ya utalii mkoani humo kwa kuwataka watumishi wa umma kufanya kazi kwa weledi, uwajibikaji na kuondoa urasimu unaoweza kukwamisha wawekezaji na wadau wa utalii.

Akizungumza na watumishi wa umma katika hafla fupi ya mapokezi iliyofanyika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Arusha Februari 10, 2026, Dk. Nguvila amesema kuwa Arusha ni lango kuu la utalii, hivyo utendaji wa watumishi unapaswa kulenga kuweka mazingira rafiki kwa uwekezaji na utoaji huduma bora kwa wadau wa sekta hiyo.

Amesisitiza kuwa kila mtumishi ana wajibu wa kuwa kichocheo cha maendeleo ya utalii kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu bila kuweka vikwazo visivyo vya lazima vinavyoweza kudhoofisha ukuaji wa sekta hiyo muhimu ya uchumi.

“Nitahakikisha hakuna urasimu wala migogoro inayokwamisha wawekezaji wa utalii. Kila wilaya ina vivutio vyake, hivyo tunapaswa kushirikiana kuvikuza kwa manufaa ya mkoa na taifa kwa ujumla,” amesema Dk. Nguvila.

Aidha, amewaagiza Wakurugenzi wa Halmashauri kutenga bajeti mahsusi kwa ajili ya shughuli za utalii, kubuni na kuimarisha vyanzo vipya vya mapato pamoja na kusimamia ukusanyaji wake kwa ufanisi.

Katika hatua nyingine, amewataka viongozi hao kuendesha kampeni za elimu na uhamasishaji wa wananchi kujiunga na Bima ya Afya kwa Wote, akieleza kuwa mpango huo utasaidia kuboresha ustawi wa wananchi na upatikanaji wa huduma za matibabu.

Awali, Dk. Nguvila alimshukuru Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kwa kumuamini na kumteua kushika wadhifa huo, akiahidi kushirikiana na wataalamu wa ngazi zote kuhakikisha wananchi wa Arusha wanapata huduma bora kwa kuzingatia sheria na miongozo ya Serikali.









Samsung Electronics East Africa imezindua rasmi maduka mawili mapya ya chapa ya Samsung katika maeneo ya Kunduchi na Ubungo, hatua inayothibitisha uwepo thabiti wa Samsung nchini Tanzania na kuimarisha ahadi yake ya kuwaletea wateja uzoefu kamili wa teknolojia inaounganisha watu wote.

Maduka haya yamefunguliwa ili wateja waweze kuona bidhaa zote za Samsung chini ya paa moja, likiweka pamoja simu za mkononi na vifaa vya elektroniki katika eneo moja. 

Kupitia Maduka haya, yanawapa wateja nafasi ya kuona na kujaribu bidhaa zote za Samsung, kutoka simu, kompyuta, televisheni, hadi vifaa vya nyumbani na vya kuvaa, na kuona jinsi zinavyorahisisha maisha ya kila siku.

Sherehe za uzinduzi zilihudhuriwa na wadau muhimu wa sekta, washirika wa biashara, pamoja na wanahabari,ikionyesha umuhimu wa uwekezaji huu kwa soko la kidijitali na rejareja Tanzania.

Akizungumza wakati wa uzinduzi, Mkuu wa Kitengo cha Simu za Mkononi wa Kampuni ya Samsung Electronics East Africa ( Tanzania) Mgope Kiwanga alisema:“Ufunguzi wa maduka haya mapya ya Kunduchi na Ubungo ni hatua muhimu katika kuwaletea wateja wetu uzoefu kamili wa Samsung.

 Hapa, wateja wanaweza kuona jinsi simu zetu na vifaa vya nyumbani vinavyoshirikiana kwa pamoja, na jinsi teknolojia inavyoweza kufanya maisha kuwa rahisi na yenye kuleta maana kila siku,” alisema Kiwanga.

Tofauti na maduka ya kawaida, maduka haya ni makubwa na yametengenezwa kwa lengo la kuleta utofouti wa bidhaa za Samsung. Hapa wateja wanaweza kuona bidhaa zote pamoja, kujaribu na kuelewa jinsi zinavyorahisisha mawasiliano, burudani na shughuli za nyumbani.

Maduka pia yanatoa elimu kwa vitendo ya namna ya kutumia Vifaa vya Samsung  , msaada wa kitaalamu kutoka kwa wafanyakazi waliofunzwa na Samsung, upatikanaji wa vifaa halisi na huduma bora baada ya mauzo, ili wateja sio tu wanunue bidhaa, bali pia kuelewa jinsi ya kutumia kikamilifu bidhaa za Samsung.

Meneja wa Kitengo Cha Biashara kutoka Samsung Tanzania Daesong Ra alsema uwekezaji huu ni endelevu unalenga kuchangia mageuzi ya kidijitali na ukuaji wa Uchumi nchini Tanzania: “Ufunguzi wa maduka haya mawili unaonyesha imani ya Samsung katika soko la Tanzania. 

Uwekezaji kama huu unapanua upatikanaji wa teknolojia, kuunda ajira na kuendeleza ujuzi wa wafanyakazi wa hapa, jambo ambalo ni muhimu kwa maendeleo ya taifa,” alisema Daesong Ra.

Mbali na kuboresha uzoefu wa wateja, maduka haya mapya pia yanachangia ukuaji wa uchumi wa ndani kupitia ajira na mafunzo kwa wafanyakazi wa Tanzania, ikiwajengea ujuzi wa hali ya juu kama Samsung-certified, kuhakikisha huduma bora na kuendeleza vipaji vya ndani.

Maduka haya mapya yanathibitisha ahadi ya Samsung kwa wateja wake Tanzania, huku wateja wakiwa na nafasi ya kupata uzoefu wa bidhaa zote na teknolojia mpya kwa urahisi.




 


Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma 

Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu  Sera , Bunge ,Uratibu na Wenye Ulemavu  Ummy Nderiananga  amesema Tanzania inaungana na nychi nyingine duniani katika kuadhimisha siku ya Kimataifa ya Breli na maadhimisho hayo hufanyika katika halmashauri zote nchini kwa ngazi ya Kitaifa .

Mh. Ummy ameogeza kuwa maadhimisho hayo yatafanyika Kitaifa  katika  Mkoa wa Tanga na kuhusisha shughuli mbalimbali ikiwemo Maonyesho ya teknolojia na kazi za wasioona, upimaji wa elimu na Ujenzi  wa wasioona, kongamano la wadau na jamii ya na shughuli za burudani na hotuba na viongozi wa Serikali na wadau. 

Mh. Ummmy amezungumza hayo kuelekea maadhimisho ya siku ya  Breli nchini yatakayofanyika  Mkoani Tanga tarehe 12 February 2026 akiwa na waandishi wa habari katika  ukumbi wa ofisi hizo jijini Dodoma leo,  akitoa tamko hilo huku  kauli mbiu ya Shughuli hiyo ni "Teknolojia ya breli husaidia kuchochea kwa wasioona na ujenzi wa Taifa."

Nderiananga ameongeza kuwa serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeendelea kuchukua hatua mbalimbali za wenye ulemavu hususani wasioona wanapata haki ,fursa na huduma sawa kama wananchi wengine ikiwemo kiuchumi,kijamii,kisiasa na kitamadu hi pia kuwapa sera ya Taifa  ya maendeleo ya huduma na mafunzo ya mwaka 2004 sera ya Elimu ya Taifa mafunzo ya 2014 toleo la  2023, sera ya ajira ya mwaka 2008 pamoja na utekelezaji wa sheria ya watu wenye ulemavu.

Kwa upende wake katibu wa chama cha wasioona Mkoa wa Dodoma Enock Mbawa amesema ushiriki wa watu wenye ulemavu unafanya watu wengine waamke kwa kusoma kwa bidii kufanya kazi kwa bidii  na kujitoa katika makongamano mbalimbali ambayo ya nahusisha watu wasioona na walemavu wengine mfano Naibu Waziri Nderiananga na kuelekeza pongezi nyingi kwa Mhe.Dkt. Samia Suluhu Hassan  Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.



 

Mkaguzi Msaidizi wa Polisi, Abel Paul, ametoa shukrani za dhati kwa wadau wote wa sekta ya habari kwa ushirikiano wao mkubwa uliowezesha kukamilika kwa utafiti wake wa kitaaluma. Kwa namna ya kipekee, ameishukuru Clouds Media Group (CMG), Millard Ayo pamoja na wanahabari na watumishi wote wa vyombo vya habari kwa mchango wao muhimu katika kufanikisha zoezi hilo.

Abel amesema kuwa ushirikiano huo ulikuwa nguzo imara katika kukamilisha utafiti huo, hasa ukizingatia unyeti na nafasi kubwa ya sekta ya habari katika jamii. Ameeleza kuwa utafiti huo ulikuwa sehemu ya mahitaji ya shahada ya uzamili katika masuala ya ulinzi wa taarifa na utawala bora, ambapo alijikita kuchambua kwa kina usalama wa taarifa, maadili ya taaluma ya habari, pamoja na mifumo ya uwazi na uwajibikaji.

Aidha, ameeleza kuwa matokeo ya utafiti wake yamekuja na mapendekezo ya kitaalamu yatakayosaidia kuboresha uendeshaji na uripoti wa masuala ya kihabari, si tu nchini Tanzania bali pia kimataifa. Amebainisha kuwa utafiti huo umejibu baadhi ya changamoto zinazoikabili sekta ya habari na kutoa dira ya maboresho yenye tija kwa wadau wote.

Akihitimisha, Abel amesisitiza kuwa maarifa na matokeo ya utafiti huo yatatumika kama nyenzo muhimu katika kuimarisha ulinzi wa taarifa, kukuza mawasiliano yenye tija, na kuendeleza misingi ya utawala bora kwa maendeleo endelevu ya jamii.

@abelstanfordp ✍️✍️



Katibu Mkuu wa Women Political Leaders (WPL), Neema Lugangira, amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi Claver Gatete, Katibu Mtendaji wa Tume ya Umoja wa Mataifa ya Uchumi kwa Afrika (United Nations Economic Commission for Africa).

Wawili hao wamejadiliana kuhusu mchango wa lishe katika maendeleo ya kiuchumi na umuhimu wa Serikali za Afrika kuipa lishe uzito wa kimkakati sawa na sekta nyingine za ukuaji.

Pia, wameangazia jinsi teknolojia za kidijitali na teknolojia mpya kama akili mnemba AI zinavyoweza kuharakisha maendeleo; na nafasi ya viongozi wanawake katika kuongoza ajenda hii hivyo kuchangia ukuaji wa kiuchumi barani Afrika.

Wamekutana leo jijini Addis Ababa, nchini Ethiopia.





Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma .

Mkurugenzi Halmashauri ya Jiji la Dodoma Dkt Frederick Sagamiko amesema kuwa kwa kushirikiana na Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela wako mbioni kuanzisha kituo atamizi ili kuwajenga vijana,wanawake na wenye ulemavu katika shughuli za kibiashara ili kuleta tija ya Mikopo ya asilimia 10 ya Halmashauri.

Dkt Sagamiko ameyasema hayo leo Februari 11,2026 Jijini Dodoma wakati akifungua Mafunzo ya utoaji mikopo kwa Vikundi ya asilimia 10 kwa kutumia mfumo jumuishi inayoratibiwa na Halmashauri na Benki ya CRDB Foundation.

Pamoja na kuwataka washiriki hao kuwa mabalozi kwa makundi mengine kujua kuwa fedha hizo wanaweza kuzipata lakini ni vema kufuata taratibu muhimu ikiwemo taarifa sahihi za eneo la biashara na kukwepa udanganyifu kama vile kuweka watu wasio sahihi katika kikundi ikiwemo Watumishi wa Umma ambao sio wanufaika.

"Kwa kushirikiana na wenzetu wa Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela tunakuja kuanzisha kituo atamizi kwaajili ya makundi ya vijana,wanawake na wenye ulemavu kwaajili ya kuwajenga kwenye shughuli mbalimbali za kibiashara ili tuone tija ya mikopo hii ya asilimia 10".

Aidha ameipongeza Benki ya CRDB kwa kuwa mshirika mzuri katika utekelezaji shughuli za mikopo kwani hadi kufikia Disemba 2025 Halmashauri ilipeleka Benki Shilingi milioni 434,984,000.00 ili kukopesha vikindi 20 ambavyo vimekidhi vigezo, ambapo hadi sasa vikundi hivyo 20 ikiwemo vya vijana 8,wanawake vi 4,na wenye ulemavu 8 vimekwisha patiwa mikopo yao.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya CRDB Foundation Bi Tully Mwambapa amesema kuwa mpaka sasa maombi ya vikundi 129 vya vijana, wanawake na watu wenye ulemavu yamepitishwa katika uchambuzi huku yakiwa na thamani ya zaidi ya Shilingi Bilioni Moja.

"Vikundi 58 vimethibitishwa na benki kuwa vina sifa za kupewa mikopo ya asilimia 10 vikiwa na thamani ya jumla ya zaidi ya shilingi Bilioni 1.1, kati ya vikundi hivyo, 32 tayari vimeshapatiwa mikopo yenye jumla ya thamani ya Milioni 584, 785 elfu, vikundi 13 vyenye thamani ya shilingi Milioni 199,497 elfu, vimekamilisha mchakato na kwa sasa viko katika hatua ya mafunzo kabla ya kupatiwa mikopo"

Akitoa neno la Shukurani kwa niaba ya wana vikundi wote na wanufaika wanaopata mafunzo hayo ya kupata fedha za mikopo ya asilimia 10 Magida Chimija amewataka vijana kutokuwa na mtazamo tofauti juu upataji wa mikopo hiyo kwa kudhani kuwa inatolewa kwa kufahamiana bali ni kwa kufuata taratibu na kukidhi vigezo kwani mikopo hii ni kwaajili ya wote wanaokidhi vigezo.

"Tuwe mabalozi wazuri tuwawlekeze wenzetu huko nje,kuwa ni kweli kabisa mikopo hii haina kujuana ni kufuata utaratibu uliowekwa ndipo utaweza kuifikia hii mikopo na hata kama utapewa chini ya kile ulichohitaji chukua tu kwani Benki ipo kila siku".

Tayari Halmashauri imehamisha Shilingi Milioni 183 kwenda Benki ya CRDB kwaajili ya kukopesha vikindi 13 vilivyokidhi vigezo vikiwemo vya Wanawake 5,Vijana 7 na Wenye Ulemavu 1 kutoka kata ya Ng'hong'ona, Hombolo Bwawani,Hombolo Makulu,Nzuguni,Viwandani ,Msalato na Kiwanja cha Ndege.













Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inashiriki Mkutano wa 48 wa Baraza la Mawaziri Afrika unaofanyika jijini Addis Ababa, Ethiopia kuanzia Februari 11-12, 2026. Ujumbe wa Tanzania katika mkutano huo unaongozwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe.shimiwa Mahmoud Thabit Kombo (Mb).

Mkutano huo unawakutanisha Mawaziri wa Mambo ya Nje na viongozi waandamizi kutoka nchi wanachama wa Umoja wa Afrika kujadili masuala muhimu ya maendeleo, usalama, ushirikiano wa kikanda na utekelezaji wa maamuzi ya Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali.

Akifungua mkutano huo, Mwenyekiti wa Tume ya Umoja wa Afrika (AUC), Mhe. Mahmoud Youssouf Ali, amesisitiza umuhimu wa mageuzi ya Taasisi na umuhimu wa amani na maendeleo barani Afrika kuelekea Mkutano wa 39 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa AU.

Amesema kuwa, Mageuzi yanaendelea chini ya Mpango wa 2024–2028 na kubainisha mafanikio yaliyopatikana katika kuimarisha muundo wa amani na usalama, kuhakikisha ufadhili endelevu, pamoja na kuimarisha taasisi za Umoja huo. Ameishukuru Jamhuri ya Angola kwa uongozi wake wa Baraza la Utendaji, huku Angola ikiwa ni Mwenyekiti wa Umoja huo anayemaliza muda wake.

Akizungumza katika ufunguzi wa mkutano huo, Waziri wa Mambo ya Nje wa Ethiopia Mhe. Gedion Timothewos, ameeleza kuwa mabadiliko yanayoendelea katika siasa za kimataifa yanazidi kudhoofisha misingi ya ushirikiano wa kimataifa na mfumo wa ushirikiano wa kimataifa.

Naye Katibu Mtendaji wa Tume ya Umoja wa Mataifa ya Uchumi ya Afrika (UNECA) Mhe.Clever Gatete ameongelea utafutaji fedha kwa ajili ya miradi ya maendeleo kwa nchi wanachama, kuunganisha miundombinu ya uzalishaji, kuongeza thamani ya madini na mazao, kuimarisha soko huru barabi Afrika na kutumia maarifa na teknolojia ya sasa ili kupata maendeleo.

Mkutano huo wa ngazi ya juu wa mawaziri ni sehemu ya maandalizi kwa ajili ya Kikao cha 39 cha Kawaida cha Wakuu wa Nchi na Serikali




 TUME ya Kuchunguza Matukio ya Uvunjifu wa Amani yaliyojitokeza wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025, leo Februari 11, 2026, imekutana na Profesa Palamagamba Kabudi.

Mkutano huo wa Tume na Kabudi umefanyika katika Ukumbi wa Tanganyika uliopo katika ofisi za Benki Kuu ya Tanzania (BoT) jijini, Dar es Salaam.

Miongoni mwa yaliyojadiliwa ni pamoja na namna matukio hayo yalivyoanza, athari zake kwa watu, mali na miundombinu pia ushauri wa namna ya kuondokana na matukio hayo.

Tume inaendelea kukutana na makundi mbalimbali wakiwemo waathirika wa Matukio hayo lengo ni kupata kiini cha chanzo cha matukio hayo na kuyawasilisha kwa ajili ya hatua zaidi.




▪️Benki ya Dunia yafurahishwa na mchango wa Sekta ya Madini wa kuchochea Uchumi Tanzania

📍 Cape town – Afrika Kusini

Sekta ya Madini Tanzania kupitia Kongamano la Mining Indaba 2026 imeendelea kuimarisha nafasi yake kimataifa, huku Tanzania ikiendelea kujidhihirisha kama kimbilio la uwekezaji katika Sekta ya Madini kwa kuvutia mashirika ya kimataifa, kampuni mbalimbali na wawakilishi wa kidiplomasia. 

Februari 10, 2026, Waziri wa Madini alikutana na wadau muhimu ikiwemo Benki ya Dunia katika vikao vya pembeni vya kongamano linaloendelea jijini Cape Town, Afrika Kusini, pamoja na kushiriki Mkutano wa Mawaziri wa Madini wa SADC.

Australia Yaipa Kipaumbele Tanzania Sekta ya Madini

Katika kikao kilichofanyika baina ya ujumbe wa Australia na Tanzania, Naibu Balozi wa Australia Christopher Ellinger alieleza kuvutiwa na mwenendo wa Sekta ya Madini nchini na kusema kwamba kwa kampuni za Australia, Tanzania ni moja ya machaguo ya kwanza kwa uwekezaji. Pia, amesisitiza utayari wa nchi hiyo kushirikiana na Tanzania katika kuendeleza miradi ya madini kupitia kampuni za Australia, na kuomba ufafanuzi wa Kanuni za Madini za ushirikishwaji wa Watanzania katika sekta, hasa katika utoaji wa huduma migodini.

Benki ya Dunia yaiweka Tanzania kama Msingi wa  Uwekezaji Afrika

Benki ya Dunia imetambua sekta ya madini Tanzania kama eneo la kimkakati lisilopaswa kuachwa pembeni katika juhudi za maendeleo na uwekezaji, ikiashiria uhitaji wa kuendelea kuwekeza na kushirikiana na serikali katika kuboresha mazingira ya uwekezaji na kuongeza faida za kiuchumi.

Benki hiyo imeunga mkono mpango wa Tanzania kujiimarisha katika shughuli za utafutaji na utafiti wa rasilimali madini na dhamira ya uongezaji thamani madini ndani ya nchi badala ya kutegemea uzalishaji na usafirishaji wa madini ghafi nje ya nchi. Hii inaonesha umuhimu wa sekta ya madini katika mipango ya maendeleo ya Tanzania na uhusiano wake na wadau wa kimataifa. 

Waziri wa Madini alisisiza dhamira ya Serikali kuimarisha ushirikiano wa kufanya tafiti za kina za jiosayansi ambazo zitaongeza wingi wa taarifa na kuchochea uwekezaji  nchini. Aidha, Waziri Mavunde amesisitiza umuhimu wa kipaumbele cha kuongeza thamani madini ndani ya nchi kama njia ya kuongeza manufaa yatokanayo na rasilimali madini badala ya kuuza madini ghafi kwa waongezaji thamani nje ya nchi.

UWEKEZAJI WA FARU GRAPHITE MAHENGE KULETA MAPINDUZI MAKUBWA NCHINI

Waziri wa Madini

 Anthony Mavunde, alisisitiza kwamba kaulimbiu ya “Madini ni Maisha na Utajiri” inaweka kipaumbele cha kufanya tafiti za jiosayansi na kuongeza thamani ya madini ndani ya nchi. Amesema Serikali iko tayari kushirikiana na wawekezaji wote wanaochangia maendeleo ya sekta ya madini nchini kwa kuzingatia Kanuni, Sheria na miongozo iliyowekwa.  Aliyasema hayo  alipokutana na Kampuni ya Faru Graphite inayomilikiwa kwa ubia baina ya Serikali na Kampuni ya Black Rock Mining inayotarajia kuchimba madini ya kinywe, katika eneo la Mahenge, Wilayani Ulanga, Mkoani Morogoro. Katika kikao hicho, Kampuni hiyo imetangaza maendeleo mazuri kwenye mradi huo na kuwashukuru viongozi wa Serikali kwa ushirikiano unaowawezesha kufanikisha kazi.

PLANTCOR MINING, STAMICO Mguu Sawa Kuchimba Dhahabu KIGOSI

Katika kikao na Waziri Mavunde, kampuni ya uchimbaji madini na ukodishaji wa vifaa vya uchimbaji ya Plantcor Mining yenye makazi yake nchini Afrika Kusini ambayo ipo katika hatua za mwisho za maandalizi ya kusaini Mkataba na Shirika la Madini laTaifa (STAMICO) ilimhakikishia Mhe. Mavunde kwamba mara baada ya kusaini mkataba huo wa ubia na STAMICO itaanza kushirikiana na STAMICO kuendeleza mradi wa uchimbaji madini ya dhahabu kwenye leseni inayomilikiwa na STAMICO katika eneo la Kigosi,Mkoani Geita.

Breakthrough Attorneys na Benki ya NMB washirikiana kuvutia uwekezaji Tanzania

Kampuni ya Breakthrough Attorneys na benki ya NMB, zimeshirikiana kuandaa na kutekeleza warsha ya kuitangaza sekta ya madini na kuvutia uwekezaji nchini Tanzania. Warsha hiyo iliyofanyika Februari 10, 2026 jijini Cape Town nchini Afrika Kusini na kuhudhuriwa na wadau mbalimbali wa sekta ya madini kutoka sehemu mbalimbali duniani.  Breakthrough Attorneys ni kampuni ya kisasa ya huduma za kisheria yenye makao yake Tanzania, inayotoa huduma mbalimbali za kisheria za kimataifa kwa kampuni, taasisi za fedha, taasisi za Serikali na watu binafsi.

Akizungumza katika warsha hiyo, Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde ambaye alikuwa mgeni rasmi, alieleza kuwa Tanzania inahama kutoka kumiliki rasilimali za madini pekee kwenda kushiriki kikamilifu katika mnyororo mzima wa thamani wa madini. Alisisitiza  kuwa uongezaji thamani nchini Tanzania si kikwazo bali ni fursa, na kuwaasa wawekezaji kuitumia fursa hiyo kikamilifu. Alisema kuwa uongezaji thamani madini unaodhamiriwa Tanzania ni ule unaojengwa kupitia ushirikiano, unaoendana na Dira ya Madini ya Afrika (Africa Mining Vision) na sera za viwanda ambazo ni rafiki kwa wawekezaji.

Mhe.  Mavunde alipongeza ongezeko la mchango wa taasisi za fedha nchini, akitolea mfano wa Benki ya NMB, ambayo inashirikiana kikamilifu na wawekezaji wa madini katika hatua zote za mnyororo wa thamani na inashiriki kuvutia wawekezaji ndani nan je ya nchi. “Muunganiko kati ya ufadhili wa kifedha wa ndani na wa kimataifa ni ishara muhimu inayoashiria kuwa sekta ya madini ya Tanzania ina uwezo wa kufadhiliwa, kukopesheka, na kuvutia uwekezaji," alisema Waziri Mavunde.











Na Oscar Assenga,MUHEZA

MKURUGENZI Bonde la Maji la Pangani Segule Segule amewaonya watu wanao kuchukua maji chini ya ardhi,juu ya ardhi bila kufuata utaratibu uliowekwa kisheria ikiwemo kuwa vibali kuacha mara moja kwani wakiwafikia watawakamata.

Segule aliyasema hayo wakati wa Mkutano Mkuu wa Uchaguzi wa Jumuiya ya Maji Mto Zigi uliofanyika mjini Muheza ambapo alisema iwe mtu binafsi au taasisi wanapaswa kuwa na vibali huku akiwashauri wafuate utaratibu na kuvichukua kwenye mamlaka husika .

Aliwaeleza wadau wa Jumuiya hiyo kuwa Bonde la Mto Pangani linasimamia vyanzo vilivyopo chini ya ardhi kupitia visima na katika eneo hilo watu wengi hawana ufahamu au wengine wanaelewa lakini hawafuati utaratibu uliowekwa

Aidha alisema watu hawana ufahamu wa kutosha katika eneo la visima kwamba ukipewa ridhaa na Mkurugenzi wa Halmshauri ukipewa hatia na Wizara ya Ardhi juu ya kutumia ardhi na unapotaka kutumia rasilimali maji lazima upate kibali kutoka kwenye Bonde husika na katika Kanda ya Kaskazini anayetaka kutimia maji kutoka chini ya ardhi lazima apate kibali kuyoka Bonde la Pangani.

Aidha alisema kwamba Serikali imefanya kwa nia njema na sio kuweka ugumu watu wasitumie lakini wasiposimamiana katika hilo ipo siku maji yote yatachafuliwa na yanaweza yasiwepo.

Alieleza kwamba wao hawatoi vibali pekee bali wanaratibu wachimbaji kujua wana utaalamu wa kutosha wanaanza kuratibu kwenye utafiti huyo anayefanya utafiti je ana taaluma hiyo mpaka wanapotoa kibali cha kuchimbiwa visima wanauhakika wanakuwa ni watu sahihi wanaotumia utaalamu sahihi hivyo uchimbahji wake hauwezi kuleta madhara kwenye jmii husika,

Awali akizungumza wakati akifungua mkutano huo kwa niaba ya Mkuu wa wilaya ya Muheza, Katibu Tawala wa wilaya hiyo serikali inatambua ushirikishwaji wa wadau mbalimbali katika usimamizi na uhifadhi na uendelezaji wa rasimali za maji na mazingira.

Alisema lengo kuu katika juhudi hizo ni kuhakikisha rasilimali za maji zinazopatikana kwa wingi ikiwemo ubora unaokubalika na kwa uendelevu wa matumizi ya maji kwa sasa na vizazi vijavyo.

“Niwapongeze viongozi mliomaliza muda wenu kwa kazi nzuri na kubwa mlioifanya na kusimamia uendeshaji wa jumuiya ikiwemo usimamizi wa vyanzo vya maji”Alisema

Aliongeza kwa athari za mabadiliko ya tabia ya nchi na hali ya hewa hapa nchini ikiwemo Muheza joto kali mvua hazinyeshi hayo yote yamebadilika kutokana na uharibifu wa mazingira unaoendelea.

Alisisitiza utunzaji wa mazingira ni jambo muhimu ambalo limeendelewa kupewa kipaumbele na Rais na hata alipoazimisha siku ya kuzaliwa alipanda miti hivyo kupitia jumuya hiyo waendelee kuwahamasisha watu wapande miti katika kila sikukuu zao muhimu ikiwemo kuzaliwa.

Hata hivyo alieleza kwamba kuna umuhimu wa Jumuiya hizo kuendelea kujengewa uwezo ili kuweza kutunza mazingira ikiwemo mafunzo ya mara kwa mara ili waweze kuendana na kazi na mazingira kipindi cha sasa.












Top News