Na Seif Mangwangi, Michuzi TV, Arusha

SERIKALI imeipongeza Menejimenti na uongozi wa chuo cha ufundi Arusha (ATC), kutokana na bunifu mbalimbali zinazoendelea kufanywa chuoni hapo ikiwemo ujenzi wa karakana ya kisasa kwaajili ya kufundishia na uzalishaji wa bidhaa mbalimbali.

Pongezi hizo zimetolewa na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Hussein Mohamed Omar, 24Julai 2026 jijini Arusha katika ziara yake ya kikazi chuoni hapo.

Dkt.Omar amesema ujenzi wa karakana hiyo ya kufundishia (Teaching Industry), utasaidia ongezeko kubwa la udahili wa wanafunzi chuoni hapo pamoja na kutoa fursa ya ajira kwa wanafunzi watakaopata elimu chuoni hapo.

Amesema Menejimenti ya chuo hicho chini ya Mkuu wake wa chuo Profesa Mussa Chacha pamoja na uongozi wa bodi ya chuo unastahili kupongezwa kwa kuwa umekuwa ukitafsiri sera ya Elimu kwa vitendo.

" Kwa niaba ya Serikali napenda kuwapongeza sana kuwekeza katika Ubunifu, lakini pia kwa kutafsiri sera ya Elimu kwa vitendo, ujenzi wa Karakana hii ni ubunifu wa hali ya juu, utaongeza udahili wa wanafunzi lakini pia kutoa ajira kwa wanafunzi watakaopata Elimu ya ufundi hapa hapa chuoni," amesema na kuongeza:

"Na wanafunzi wengine watakaofaulu vizuri pia wataajiriwa hapa hapa katika Karakana hii kwaajili ya kuzalisha bidhaa mbalimbali ambazo zitatumika ndani na nje ya nchi," amesema.

Dkt. Omar amesema kuwa tafsiri ya Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan ni kutafsiri Sera ya Elimu na maono ya dira ya Taifa ya 2050 ya kuhakikisha watanzania wengi wanapata elimu na Ujuzi wa kujiajiri wenyewe.

"Chuo cha Ufundi Arusha (ATC) kinaendelea kuimarisha elimu ya ufundi nchini kupitia ujenzi wa Kiwanda cha Uzalishaji (Industrial Workshop), mradi unaolenga kuwapa wanafunzi ujuzi wa vitendo, uzoefu wa kazi na kuwaandaa kwa soko la ajira," amesema Dkt Omar.

Kupitia kiwanda hicho, wanafunzi watashiriki katika uzalishaji wa bidhaa mbalimbali ikiwemo kuchonga vipuri vya magari, kupata uzoefu wa kazi, kuongeza uwezo wa kujiajiri au kuajiriwa, na hivyo kujipatia kipato wakati wa masomo.

Mkuu wa Chuo cha Ufundi Arusha, Prof. Musa Chacha, amesema mradi huo unaunga mkono Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kwa kuzalisha wahitimu wenye ujuzi unaokidhi mahitaji ya uchumi wa kisasa.

Amesema chuo chake kimeshaanza uzalishaji wa mita janja zinazotumika kusoma Dira ya maji kwa malipo ya kabla (pre paid bill), hatua inayoonyesha dhamira ya chuo kuunganisha elimu, teknolojia na maendeleo ya viwanda nchini.

Prof. Chacha amesema kiwanda hicho kitatumika pia kufanya uzalishaji wa mita hizo janja ambazo zitasambazwa kwa mamlaka za maji nchini ambazo zitakuwa tayari kuanza kuzitumia.

Meneja msimamizi wa MRADI wa Ujenzi wa kiwanda Cha Kufundishia (Teaching Industry) Mhandisi, Elineema Willium amesema mradi huo umewezeshwa na Serikali ya Tanzania kwa kushirikiana na Serikali ya Austria kupitia mkopo wa masharti nafuu.

Mhandisi Msuya amesema kuwa mradi huo umeleta manufaa makubwa kwa wanafunzi chuoni hapo,kwa kuwa wanafunzi wamejifunza Teknolojia mpya kupitia Ujenzi huo kutoka nchini Austria.






📍Ni baada ya MwanaFA kutoa fedha za kugharamia matibabu hayo


MUHEZA:

MBUNGE wa Muheza na Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Hamis Mwinjuma, maarufu kama 'MwanaFA', ametekeleza ahadi yake kwa kutoa chupa 99 za dawa ya kutibu sumu ya nyoka (antivenom) zenye thamani ya shilingi milioni 15, ili ziweze kutolewa bure kwa wananchi.

Mhe. Mwinjuma amekabidhi dawa hizo Julai 24, wakati wa kikao cha ndani cha wana CCM wa Kata za Tongwe na Nkumba, na kueleza kuwa hatua hiyo ni utekelezaji wa ahadi aliyoitoa wakati wa kampeni mwaka jana.

"Mganga Mkuu, niliahidi kwamba endapo wananchi wa Muheza watanichagua tena, dawa za sumu ya nyoka nitazitoa ili wananchi watibiwe bure. Leo nakukabidhi chupa hizi 99 zenye thamani ya shilingi milioni 15," alisema Mhe. Mwinjuma.

Wilaya ya Muheza, yenye jumla ya vijiji 126 na kata 37, imezungukwa na mazingira ya misitu ambayo hupelekea wananchi kung'atwa na nyoka mara kwa mara wanapokuwa katika shughuli zao za mashambani.

Akithibitisha ukubwa wa tatizo hilo wakati akipokea dawa hizo, Mganga Mkuu wa Wilaya ya Muheza, Dkt. Fani Mussa, alisema kwa mwaka 2024/25 pekee, jumla ya watu 108 waliripotiwa kung'atwa na nyoka, huku watu 13 kati yao wakifariki dunia.

"Tunakushukuru mbunge kwa dawa hizi, umewasaidia sana wananchi wetu hapa wilayani kufuatia kilio chao cha muda mrefu. Tutazisambaza katika vituo vyetu vya afya na zahanati na wananchi watakaoumwa na nyoka watatibiwa bure kuanzia sasa," alisema Dkt. Fani.

Inaelezwa kuwa dozi moja ya dawa hiyo inagharimu kati ya shilingi 293,000 hadi 300,000, kiwango ambacho ni kikubwa kwa wananchi wengi wa kawaida kuweza kikumudu kutokana na ugumu huo, waathirika wengi walikuwa wakilazimika kukimbilia kwa waganga wa kienyeji.

Akizungumzia msaada huo, Katibu wa CCM Wilaya ya Muheza, Simon Leng'ese, alimshukuru mbunge huyo na kumwelezea kama kiongozi mwenye utu na anayejali maisha ya wapiga kura wake.

"Mheshimiwa mbunge, kwa niaba ya CCM tunakupongeza sana. Si watu wote wenye moyo kama huo, lakini kwa kitendo hiki cha kutoa dawa, umetenda jambo kubwa ambalo Mungu tu atakulipa. Sisi wenzako wa Muheza tutahakikisha tunakuunga mkono kwa sababu wewe ni hazina ya Muheza na Taifa kwa ujumla," alisema Leng'ese.

Kwa upande wake, mmoja wa wananchi kutoka Kijiji cha Nkumba Stuart Mdachi aliyehudhuria kikao hicho, alipongeza hatua hiyo na kukiri kuwa imekuja wakati mwafaka.

"Kiukweli mbunge tuliyenaye, hiki alichofanya ni jambo kubwa sana. Wananchi wengi walikuwa wakishindwa kwenda hospitali kwa sababu walikuwa hawana shilingi laki tatu, hivyo wanaenda kwa waganga wa kienyeji au kutumia dawa za mitishamba na wakati mwingine kupoteza maisha," alisema mwananchi huyo.






Rais wa IPU afuata nyayo za kiongozi mashuhuri wa Afrika katika ziara yake rasmi ya kikazi nchini Burkina Faso, Rais wa Umoja wa Mabunge Duniani (IPU) Mhe. Dkt. Tulia Ackson ametembelea na kujionea Kituo cha Kumbukumbu cha Thomas Sankara akiambatana na Naibu Spika wa Bunge la Burkina Faso Mhe. Haoua Fofana pamoja na wajumbe wa wabunge.

Wakati wa ziara hiyo, Rais wa IPU ametembelea maeneo mbalimbali ya kituo hicho na kuona alama zinazoakisi safari, misingi ya mawazo na dhamira ya Kapteni Thomas Sankara katika kuwakomboa watu wake na bara la Afrika.

Waongoza wageni wametoa maelezo ya kina kuhusu hatua muhimu za maisha ya Thomas Sankara mazingira yaliyochochea harakati zake za kisiasa na athari endelevu za urithi wake, maelezo hayo yameupa wajumbe hao uelewa mpana zaidi wa historia inayomzunguka shujaa huyo wa Burkina Faso.

Akiwa ameguswa sana kihisia, Dkt. Tulia Ackson ameeleza kuwa ni heshima kubwa kuwepo katika eneo lenye historia nzito na muhimu, amebainisha kuwa ingawa historia ya Thomas Sankara inajulikana sana kupitia vitabu, majarida na vyombo vya habari, kuishuhudia ana kwa ana kunaleta hisia za kipekee.

Ziara hii katika kituo cha kumbukumbu cha Thomas Sankara imempa Rais wa IPU Mhe. Dkt. Tulia Ackson uelewa bora zaidi wa nafasi ambayo Kapteni Thomas Sankara anaendelea kuwa nayo katika kumbukumbu za watu iwe ni nchini Burkina Faso au kimataifa.









Na Mwandishi Wetu

KAMPENI maalum ya Kuwa Makini Okoa Maisha kwa madereva bodaboda maarufu kama maofisa usafirishaji imeanza rasmi mkoani Dar es Salaam lengo likiwa ni kuwapatia mafunzo ya elimu ya usalama barabarani pamoja na vifaa kinga kama sehemu ya kukomesha ajali za barabarani.

Akizungumza kuhusu kampeni hiyo leo Julai 25,2025 na maofisa usafirishaji katika eneo la Tangi Bovu -Kawe wilayani Kinondoni mkoani Dar es Salaam Rais wa Chama cha Watalaam wa Afya na Usalama Mahala Pa kazi Tanzania(TOHASA) Caroline Baraza amesema wameamua kuja na kampeni hiyo ya kuwapatia elimu hiyo ya usalama barabarani ili kupunguza ajali.

“Lengo ni kuwapatia elimu maofisa usafirishaji ili wawe makini na kuheshimu sheria kwasababu tunaangalia ajali nyingi zinazotokea na takwimu zinaonesha watu wengi wanakosa elimu na kutokujua wafanye nini wakati gani lakini lengo kuu ni kuokoa maisha ndio maana hizi Reflecta zetu zimeandikwa kuwa makini okoa maisha hiyo ndio kauli mbiu yetu tunayokwenda nayo .

“Mwito wa TOHASA kwa maofisa usafirishaji wafuate sheria za barabarani kwani hazina mtu huyu na huyu bali ziko kwa ajili yetu sote tunaotumia barabara.Pia kuwa makini pale inapobidi unapoona mwenzako anavunja sheria wewe kuwa makini na mfundishe au kumuekeleza.”

Amesema katika chama hicho wameshirikiana na wadau mbalili na wakiwemo OSHA WCF, Safety and Security, Jafferjee na TMHS group

Kwa upande wake Mkuu wa usalama barabarani Wilaya ya Polisi Kawe/Mbweni Mkoa wa Kinondoni Adrian Kamara amesema kupitia kampeni ya TOHASA wametoa elimu kwa maofisa usafrishaji katika kituo cha Tangi Bovu.

“Tumeshirikiana na TOHASA ambao wanahusika na usalama mahala pa kazi kuwakumbusha madereva pikipiki kuzingatia usalama na abiria pamoja na utumiaji sahihi wa barabara ,watii sheria za usalama barabarani kwa maana ya kuheshimu vivuko ,kutoendesha pembeni ya barabara.

“Tumewafahamisha wao ni watumiaji rasmi na wanatambulika kisheria hivyo waendeshe pikipiki zao katikati ambako ni sehemu sahihi kama ni kushoto au kulia kufuata utaratibu kama magari yanavyotembea kwani dereva makini hawezi kumparamia mwendesha pikipiki”

Pia amesema wamewasisitiza lakini uvaaji wa viakisi mwanga (Reflekta) ili waweze kuonekana nyakati za usiku au wanapoendesha katika maeneo yenye uono hafifu kwa madereva wengine wa barabara .Wamewakumbusha uvaaji kofia ngumu bila kujali umri lakini TOHASA imewapa reflecta viakisi mwanga pamoja na mawani kwa ajili ya kujikinga na vumbi.

Wakati huo huo Gerald Mrema ambaye ni Makamu wa Rais wa TOHASA amesema wameamua kufanya kampeni hiyo kwasababu kuna ongezeko la vifo vinavyotokana na ajali za barabarani ,majeruhi pamoja na ulemavu wa kudumu hivyo wao wameamua kama taasisi ya usalama mahala pa kazi kujikita kuwapa elimu hiyo.

“Taasisi yetu kwa kushirikiana na Jeshi la

Polisi pamoja na taasisi mbalimbali ambazo zinatoa vifaa kinga vya usalama pahala pa kazi tumetoa elimu kwa bodaboda tukiwa na kusudi kubwa baada ya elimu hii watahakikisha wanaendesha vyombo vya moto kwa kuzingatia sheria na taratibu za nchi kwa kufuata alama za barabarani kwa kutopakia abiria zaidi ya mmoja,”amesema Mrema.

Aidha amesisitiza umuhimu wa madereva bodaboda kuhakikisha wanavaa vifaa kinga wanapokuwa mahala pa kazi kwa mfano reflekta ili waonekane kwa mbali lakini kuvaa viatu kinga ambavyo ajali iwapo itatokea vitalinda miguu yao sambamba na utaratibu wa ukaguzi wa vyombo vyao vya moto mara kwa mara asubuhi kabla ya kuanza kutumia ili kuona kama chombo ni salama kwa ajili ya matumizi.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Tangi Bovu Shule Athuman Kitunguu amesema wanashukuru kwa kupatiwa elimu ya usalama barabarani pamoja na vifaa kinga huku akieleza kumekuwepo na changamoto nyingi ikiwemo ajali za barabarani na kwamba Jeshi la Polisi kupitia elimu wanazotoa sasa wanathaminiwa ikilinganishwa na hapo awali.

“Kwasasa tunashukuru Jeshi la Polisi limepoa na wanatupa ushirikiano mzuri na elimu ambazo tunapatiwa zinatuongezea uelewa kuhusu kuhusu kufuata sheria za usalama barabarani.”













Na. Saidina Msangi, WF, Abidjan.

Nchi za Afrika zimekubaliana kuweka kipaumbele katika ufadhili wa viwanda vinavyotegemea rasilimali za ndani ikiwemo madini na kuhakikisha kuwa zinaongeza thamani ya bidhaa na kuimarisha biashara ya ndani ya bara ili kujenga maendeleo jumuishi, endelevu na yenye tija.

Hayo yalibainishwa na Naibu Waziri wa Fedha, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), baada ya kuhitimishwa kwa Mkutano wa Pamoja wa 9 wa Kamati Maalum ya Mawaziri (STC) ya Umoja wa Afrika inayosimamia masuala ya Fedha, Uchumi, Mipango na Mtangamano pamoja na Mkutano wa 5 wa Kamati Maalum ya Mawaziri inayosimamia masuala ya Biashara, Utalii, Viwanda na Madini, uliofanyika jijini Abidjan, nchini Côte d’Ivoire.

Mhe. Munde alisema hatua hiyo inalenga kuharakisha mageuzi ya uchumi kwa kuongeza thamani ya rasilimali zilizopo, kuimarisha ushirikiano wa kikanda ili kupunguza utegemezi kutoka kwa wafadhili.

‘‘Afrika ina utajiri mkubwa wa madini, biashara na utalii ambazo ni nguzo kuu zinazoweza kukuza uchumi kama kutawekwa uratibu mzuri na madhubuti baina ya mataifa wanachama, na kuweka mikakati ya kusimamia ustahimilivu wa madeni ya taifa ili kupunguza utegemezi wa kifedha kutoka kwa wadau wa nje’’, alisema Mhe. Munde.

Aidha, Mhe. Munde alisema Afrika ina nguvu kazi ya vijana wenye ubunifu na nguvu ambapo wakiwezeshwa kupitia uboreshaji wa mifumo ya elimu na mafunzo ya ujuzi, pamoja na kuweka mazingira ya kutumia teknolojia mpya na za kisasa kama Akili unde (AI) itawezesha kuwa na nguvu kazi yenye ushindani wa kimataifa na kuchochea mapinduzi ya viwanda na kiuchumi barani Afrika.

‘‘Katika kukuza biashara ya kikanda, tulijadili umuhimu wa kuondoa vikwazo vyote vya ushuru na visivyo vya ushuru, kufanyia marekebisho sheria na sera za nchi zilizokuwa zikibagua wafanyabiashara wa Afrika pamoja na kuimarisha na kujenga shoroba mpya za kiuchumi zitakazounganisha nchi na nchi, ili kuwezesha mzunguko huru wa watu, bidhaa, na huduma kupitia Eneo la Biashara Huru la Afrika (AfCFTA)’’, alifafanua Mhe. Munde.

Awali akizungumza wakati akichangia mada, Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Dennis Londo, alisema ili kuharakisha mageuzi ya kiuchumi Afrika ni muhimu kuimarisha ujumuishaji wa kifedha, kuendeleza shoroba za kiuchumi, pamoja na kuweka mifumo bora ya usafirishaji na ugavi ili kuongeza ushindani katika masoko ya kikanda na ya kimataifa.

‘‘Ili kufikia azma hii, ni lazima kuratibu sera za udhibiti na kushughulikia vikwazo vya biashara ya mipakani, ikiwa ni pamoja na kurahisisha usafirishaji wa bidhaa, uhuru wa watu kusafiri, na kuwekeza katika miradi ya kimkakati ya miundombinu kama vile barabara, reli, bandari na njia za maji ili kuunganisha nchi zetu na kurahisisha mwingiliano wa watu, bidhaa na huduma’’, alisema Mhe. Londo.

Alisisitiza kuwa kuunganisha maeneo ya uzalishaji wa mazao ya kilimo na madini na vituo vya uchakataji, Afrika itaweza kujenga minyororo imara ya thamani ya kikanda na kuongeza mauzo ya bidhaa zilizochakatwa zenye kukidhi viwango vya kimataifa, badala ya kuendelea kuuza malighafi pekee.

Mkutano huo uliofanyika kwa siku mbili uliokuwa na kaulimbiu "Kufadhili Maendeleo ya Viwanda barani Afrika kwa Maendeleo Endelevu" (Financing Africa's Industrialization for Sustainable Development), ulilenga kuongeza kasi ya maendeleo ya viwanda vinavyotegemea rasilimali za madini barani Afrika.


Naibu Waziri wa Fedha, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), akiagana na Waziri wa Maliasili na Nishati wa Eswatini ambaye pia ni Kaimu Mwenyekiti wa Mkutano wa 5 wa Kamati Maalum ya Mawaziri inayosimamia masuala ya Biashara, Utalii, Viwanda na Madini, Mhe. Prince Damian, baada ya kuhitimishwa kwa Mkutano wa Pamoja wa 9 wa Kamati Maalum ya Mawaziri (STC) ya Umoja wa Afrika inayosimamia masuala ya Fedha, Uchumi, Mipango na Mtangamano pamoja na Mkutano wa 5 wa Kamati Maalum ya Mawaziri inayosimamia masuala ya Biashara, Utalii, Viwanda na Madini, jijini Abidjan, nchini Côte d’Ivoire.




Naibu Waziri wa Fedha, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), akiongoza Mkutano kuthibitisha maazimio ya kikao, katika Mkutano wa Pamoja wa 9 wa Kamati Maalum ya Mawaziri (STC) ya Umoja wa Afrika inayosimamia masuala ya Fedha, Uchumi, Mipango na Mtangamano pamoja na Mkutano wa 5 wa Kamati Maalum ya Mawaziri inayosimamia masuala ya Biashara, Utalii, Viwanda na Madini, jijini Abidjan, nchini Côte d’Ivoire.


Naibu Waziri wa Viwanda, Mhe. Dennis L. Londo, akichangia mada katika Mkutano wa Pamoja wa 9 wa Kamati Maalum ya Mawaziri (STC) ya Umoja wa Afrika inayosimamia masuala ya Fedha, Uchumi, Mipango na Mtangamano pamoja na Mkutano wa 5 wa Kamati Maalum ya Mawaziri inayosimamia masuala ya Biashara, Utalii, Viwanda na Madini, jijini Abidjan, nchini Côte d’Ivoire.








Naibu Waziri wa Madini Mhe. Dkt. Steven Lemomo Kiruswa, akichangia mada katika Mkutano wa Pamoja wa 9 wa Kamati Maalum ya Mawaziri (STC) ya Umoja wa Afrika inayosimamia masuala ya Fedha, Uchumi, Mipango na Mtangamano pamoja na Mkutano wa 5 wa Kamati Maalum ya Mawaziri inayosimamia masuala ya Biashara, Utalii, Viwanda na Madini, jijini Abidjan, nchini Côte d’Ivoire.


Naibu Waziri wa Fedha, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), akipongezwa na Naibu Waziri wa Viwanda, Mhe. Dennis Londo, (kulia), na Naibu Katibu Mkuu Mtendaji, Tume ya Taifa ya Mipango, Dkt. Blandina Kilama (wa pili kulia), baada ya kuhitimishwa kwa Mkutano wa Pamoja wa 9 wa Kamati Maalum ya Mawaziri (STC) ya Umoja wa Afrika inayosimamia masuala ya Fedha, Uchumi, Mipango na Mtangamano pamoja na Mkutano wa 5 wa Kamati Maalum ya Mawaziri inayosimamia masuala ya Biashara, Utalii, Viwanda na Madini, jijini Abidjan, nchini Côte d’Ivoire.




(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, WF, Abidjan, Côte d’Ivoire.)

Na Benny Mwaipaja, London

Tanzania imeandika historia mpya katika masoko ya fedha ya kimataifa baada ya hatifungani ya kwanza inayotolewa nje ya nchi (Tanzania off-shore Bond) yenye thamani ya dola za Marekani milioni 100, sawa na takriban shilingi bilioni 262.5 za Tanzania, iliyotolewa na Shirika la Fedha la Kimataifa, mwanachama wa Kundi la Benki ya Dunia (IFC) kwa kutumia sarafu ya Tanzania, kuorodheshwa katika Soko la Hisa la London, Uingereza.

Fedha hizo zimeekezwa Benki ya NMB Plc kwa njia ya mkopo, ambako zitatumika kuwaendeleza kimtaji wafanyabiashara wadogo na wa kati (MSMEs), huku asilimia 20 ya fedha hizo sawa na takriban shilingi bilioni 52.5 zimetengwa kwa ajili ya kuwawezesha wafanyabiashara wadogo wanawake.

Akizungumza kuhusu hatua hiyo, baada ya kupiga kengele kuashiria uzinduzi wa hati fungani hiyo na kufunga biashara ya soko la hisa kwa siku hiyo, Waziri wa Fedha wa Tanzania, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar, alisema mafanikio hayo yanafungua ukurasa mpya wa kuiwezesha Tanzania kujenga imani zaidi kwa wawekezaji wa kimataifa na kupanua vyanzo vya mitaji kwa ajili ya Dira 2050.

“Huu ni mwanzo wa hatua muhimu katika safari ya Tanzania ya kushiriki kikamilifu katika masoko ya mitaji ya kimataifa kwa kutumia sarafu yetu wenyewe. Uorodheshwaji huu unaonesha imani kubwa ya taasisi za kifedha za kimataifa kwa uchumi wetu na mwelekeo wa mageuzi ya sekta ya fedha nchini,” alisema Mhe. Balozi Omar.

Aidha, Mhe. Balozi Omar alisema kuwa uorodheshwaji wa hatifungani hiyo katika soko kubwa na lenye hadhi duniani kama London Stock Exchange, unaipa Tanzania thamani ya kipekee ya sifa na ishara chanya kwa wawekezaji, jambo litakalosaidia kuboresha uwezo wa nchi kukopa na kukopesheka kwa gharama nafuu.

“Lengo letu si tu kuona dhamana hii inafanikiwa katika soko la kimataifa, bali pia kuhakikisha kuwa matokeo yake yanaonekana moja kwa moja katika ukuaji wa sekta binafsi, hususan kwa wafanyabiashara wadogo na wa kati ambao ni nguzo muhimu ya uchumi wetu,” alisema Mhe. Balozi Omar.

Naye Mkurugenzi Mtendaji na Afisa Mtendaji Mkuu wa NMB, Bi. Ruth Zaipuna, alieleza furaha yake kuhusu hatua hiyo na kwamba fedha zilizopatikana zitasaidia kuchachua uchumi wa nchi kwa kutoa mikopo ya muda mrefu kwa wafanyabiashara wadogo, wa kati, jambo litakaloongeza kasi ya ukuaji wa sekta binafsi, ajira na shughuli za uzalishaji nchini.

“Hii ni mara ya pili kwa benki yetu kunufaika na Soko la Hisa la London ambapo mwaka 2023 tulipata zaidi ya shilingi bilioni 400 kupitia Hati Fungani ya Jamii na sasa tumepata zaidi ya shilingi bilioni 262.5 kupitia hati Fungani ambayo kwa mara ya kwanza imeorodheshwa kwa sarafu ya Tanzania” Alisema Bi. Zaipuna.

Kwa Upande wake, makamu wa Rais wa Benki ya Dunia anayesimamia masuala ya Hazina, Bw. Jorge Familiar, alisema kuwa Benki ya Dunia inajisikia fahari kushirikiana na Tanzania kutimiza malengo yak ya kukuza uchumi wake jumuishi kupitia utekelezaji wa Dira ya taifa ya Maendeleo 2050.

“Tunacho kiangalia sisi si tu kiwango cha fedha tunachowekeza kwa kushrikiana na washirika wetu bali ni matokeo ya uwekezaji huu ambapo tunaamini fedha hizi zitaleta mageuzi makubwa ya kiuchumi na kijamii na tunakadiria kuwa zaidi ya watu elfu 13 hadi 20 wakiwemo wanawake watapata ajira na wakati huo huo wawekezaji wa kimataifa wamepata nafasi ya kuwafikia wafanyabiashara kwa kuwekeza” alisisitiza Bw. Familiar.

Kwa ujumla, uorodheshwaji wa hatifungani hiyo unatajwa kuwa ni hatua ya kimkakati inayoiweka Tanzania katika nafasi bora zaidi ya kushindana katika soko la kimataifa la fedha, huku ukiunga mkono jitihada za kukuza uchumi jumuishi na endelevu.

Benki ya Dunia kupitia Taasisi yake ya IFC, imewekeza nchini Tanzania zaidi ya dola za Marekani bilioni 1.6 ambazo zimekezwa katika miradi mbalimbali ya kimkakati inayokwenda sambamba na malengo ya serikali kuitia seka binafsi katika miradi ya miundombinu, kilimo, masoko ya mitaji na nishati.


Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), (wa nne kutoka kulia) akizindua Hatifungani ya kwanza inayotolewa nje ya nchi (offshore) yenye thamani ya dola za Marekani milioni 100, sawa na takriban shilingi bilioni 262.5 za Tanzania, iliyotolewa na Shirika la Fedha la Kimataifa, mwanachama wa Kundi la Benki ya Dunia (IFC) kwa kutumia sarafu ya Tanzania, iliyoorodheshwa katika Soko la Hisa la London, Uingereza ikiwa ni mkopo kwa Benki ya NMB kwa ajili ya kuwakopesha wafanyabiashara wadogo na wa kati. Miongoni mwa wanaoshuhudia ni Mkurugenzi Mtendaji na Afisa Mtendaji Mkuu wa NMB Bank Bi. Ruth Zaipuna (wa sita kulia) na Makamu wa Rais wa Benki ya Dunia-Hazina, Bw. Jorge Familiar (wa tatu kulia).

Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (kushoto), akiwa na Makamu wa Rais wa Benki ya Dunia-Hazina, Bw. Jorge Familiar, baada ya kuzinduliwa kwa Hatifungani ya kwanza inayotolewa nje ya nchi (offshore) yenye thamani ya dola za Marekani milioni 100, sawa na takriban shilingi bilioni 262.5 za Tanzania, iliyotolewa na Shirika la Fedha la Kimataifa, mwanachama wa Kundi la Benki ya Dunia (IFC) kwa kutumia sarafu ya Tanzania, iliyoorodheshwa katika Soko la Hisa la London, Uingereza ikiwa ni mkopo kwa Benki ya NMB kwa ajili ya kuwakopesha wafanyabiashara wadogo na wa kati.




Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), (wa Sita kutoka kulia) akisikiliza maelezo kutoka kwa Afisa Mtendaji Mkuu wa Soko la Hisa la London, Bi. Julia Hoggett (wa nne kulia), wakati wa kuzindua Hatifungani ya kwanza inayotolewa nje ya nchi (offshore) yenye thamani ya dola za Marekani milioni 100, sawa na takriban shilingi bilioni 262.5 za Tanzania, iliyotolewa na Shirika la Fedha la Kimataifa, mwanachama wa Kundi la Benki ya Dunia (IFC) kwa kutumia sarafu ya Tanzania, iliyoorodheshwa katika Soko la Hisa la London, Uingereza ikiwa ni mkopo kwa Benki ya NMB kwa ajili ya kuwakopesha wafanyabiashara wadogo na wa kati.
(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini-WF-London)





















WAKULIMA zaidi ya 650 katika kijiji cha Kipande-Nkoavele, Halmashauri ya Meru katika Mkoa wa Arusha kunufaika na mita 1000 za mifereji ya umwagiliaji kwa gharama ya Shilingi Milioni 200 ili kuendeleza matumizi ya kilimo cha umwagiliaji cha mazao ya mboga mboga na matunda.

Amesema hayo Waziri wa Kilimo, Mhe. Daniel Chongolo (Mb) tarehe 24 Julai 2026 na kuielekeza Tume ya Taifa ya Umwagiliaji (NIRC) kukaa na timu yake ya Mkoa ili kuanza kazi ya kuongeza mfereji huo.

Mita hizo 1000 zinaenda kuongezwa na Tume ya Taifa ya Umwagiliaji kwenye ujenzi wa awali wa mifereji yenye urefu wa mita 612 iliyogharimu Shilingi Milioni 188.9 zilitolewa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii TASAF kupitia mfuko wa OPEC II, III na IV. 

Katika hatua nyingine, Mhe. Waziri Chongolo ameielekeza Mamlaka ya Udhibiti wa Nafaka na Mazao Mchanganyiko (COPRA) kujenga soko la kisasa ndani ya miezi saba (7) lenye sehemu ya uhifadhi wa baridi ili mazao ya mboga mboga na matunda yanayovunwa yaweze kuhifadhiwa kuepusha kuharibika kwa haraka.  

Sambamba na hilo, Kampuni ya Mbolea Tanzania (TFC) imetoa ahadi kwa wakulima wa Halmashauri ya Meru kuwa itapeleka mbolea mapema hivi karibuni ili wakulima waweze kuongeza uzalishaji wa mazao kwa ubora zaidi.

















WANANCHI wa Wilaya ya Arumeru, Mkoani Arusha wamepewa shimishimi ya kuendelea na shughuli za kiuchumi kwa kuwa ahadi za Serikali kuwaletea maendeleo zitatekelezwa.

Amesema Waziri wa Kilimo, Mhe. Daniel Chongolo (Mb) wakati wa ziara yake ya kikazi mkoani Arusha tarehe 24 Julai 2026 ambapo amekagua utekelezaji wa miradi ya maendeleo ambayo ni barabara wa KIA-Usa River; ujenzi wa skimu ya umwagiliaji ya kijiji cha Kipande-Nkoavele; uzinduzi wa mabweni, madarasa na vyoo katika Shule ya Sekondari ya Mlangarini na mkutano wa hadhara wa eneo la Usa River.

Amepongeza wananchi hao ambao asilimia 90 ni wakulima wa kilimo cha umwagiliaji cha mazao ya mboga mboga na matunda (horticulture) katika Halmashauri ya Meru.

“Nimewasikia kilio chenu cha kuongezewa mita 1000 za mifereji ya umwagiliaji hivyo nimeielekeza Tume ya Taifa ya Umwagiliaji (NIRC) kutoa Shilingi Milioni 200 kugharamia ujenzi huo,” amesema Waziri Chongolo.

Kuhusu ombi la kujengewa soko na chumba cha ubaridi cha kuhifadhi mazao, Waziri Chongolo ameielekeza Mamlaka ya Udhibiti wa Nafaka na Mazao Mchanganyiko (COPRA) kufanya taratibu za ujenzi wa soko hilo ndani ya miezi saba (7).

Wakati wa ziara yake, Waziri Chongolo amekagua pia barabara wa KIA-Usa River; ujenzi wa skimu ya umwagiliaji ya kijiji cha Kipande-Nkoavele; uzinduzi wa mabweni, madarasa na vyoo katika Shule ya Sekondari ya Mlangarini na kufanya mkutano wa hadhara na mamia ya wananchi waliojikusanya katika eneo la Usa River.

Viongozi mbalimbali walioshiriki katika ziara hiyo ni pamoja Katibu Tawala Mkoa wa Arusha, Dkt. Toba Alnason Nguvila; Mkuu wa Wilaya ya Arumeru, Mhe. Mwinyi Ahmed Mwinyi; Mbunge wa Arumeru Mashariki, Mhe. Joshua Nassari; Mbunge wa Arumeru Magharibi, Mhe. Dkt. Johannes Lembulung Lukumay; Wakurugenzi wa Wizara ya Kilimo na Taasisi zake.




















Top News