Na Vero Ignatus, Michuzi TV-Arusha

Serikali imeeleza kuwa ina matarajio makubwa kwa Mawakili wa Serikali katika kuhakikisha utekelezaji wa miradi ya kimkakati inayolenga kufanikisha Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050,

Matarajio hayo yameelezwa na Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Zainab Katimba, wakati akifunga mafunzo ya siku tatu ya Mawakili wa Serikali yaliyofanyika jijini Arusha kuanzia Julai 15 hadi 17, 2026.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Katimba amewataka Mawakili wa Serikali kuyatumia mafunzo hayo kuboresha utendaji wao wa kazi, ikiwemo kutoa ushauri wa kisheria, kuandaa na kupitia mikataba, kusimamia majadiliano ya kimkakati pamoja na kushughulikia mashauri kwa weledi na ufanisi.

Amesema Serikali inahitaji Mawakili wa Serikali wenye uwezo wa kuona mbali, kufikiri kimkakati na kutumia sheria kama nyenzo ya maendeleo ili kuhakikisha kila uamuzi wa Serikali unalinda maslahi ya Taifa, unakuza uchumi na kuchochea utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

"Imani yangu kwenu ni kubwa kuwa ninyi mliohudhuria mafunzo haya mtakuwa sehemu ya kizazi cha Mawakili wa Serikali kitakachoiwezesha Taifa kufikia matarajio makubwa ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050," amesisitiza Mhe. Katimba.

Awali akimkaribisha mgeni rasmi, Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Samwel M. Maneno, alisema mafunzo hayo yamewapa washiriki fursa ya kujadili na kujifunza masuala mbalimbali ya kimkakati yatakayowawezesha kutekeleza majukumu yao kwa weledi, ubunifu na ufanisi zaidi katika kulinda na kutetea maslahi ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mhe. Maneno alieleza kuwa mafunzo hayo yalijikita katika usimamizi wa majadiliano na mikataba ya kimkakati, usuluhishi wa migogoro, ubia kati ya sekta ya umma na binafsi (PPP), usimamizi wa vihatarishi vya kisheria (Legal Risk Management), pamoja na matumizi ya Akili Unde (AI) katika taaluma ya sheria.

Aidha, aliwataka Mawakili wa Serikali kuendelea kutekeleza maelekezo yaliyotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, wakati wa ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Chama cha Mawakili wa Serikali (TPBA) 2026. 

Pia aliwasisitiza kusoma na kutafakari kwa kina kitabu cha Mama Samia Doctrine of Law ili kuelewa falsafa ya uongozi wa Rais na kuongeza kasi pamoja na ubora katika uchakataji wa masuala ya kisheria, hususan upekuzi na uandaaji wa mikataba kwa kuzingatia sheria, kanuni, miongozo na maslahi ya Taifa.

Mafunzo hayo ya Bespoke 2026 yalifanyika chini ya kaulimbiu "Repositioning State Attorneys for Strategic Legal Leadership in Realizing Tanzania Development Vision 2050," yakihusisha Mawakili wa Serikali kutoka Wizara, Idara Zinazojitegemea, Wakala za Serikali pamoja na Mamlaka za Serikali za Mitaa (RS na LGAs) kwa lengo la kuimarisha uongozi wa kisheria katika kufanikisha Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.








Na Seif Mangwangi, Michuzi TV Arusha

SERIKALI ya Mapinduzi Zanzibar imesema ina mikakati ya kuleta madereva kutoka visiwani humo kuja katika chuo cha ufundi Arusha (ATC), kujifunza ujuzi wa kuendesha magari tofauti ikiwemo ya viongozi na kuepusha ajali zinazotokea mara kwa mara.

Hayo yameelezwa na Naibu Waziri wa wizara ya ujenzi na uchukuzi Zanzibar, Badria Atai Masoud, Julai16, 2026 alipofanya ziara katika chuo cha ufundi Arusha na kujionea mitambo mbalimbali inayotumika kufundishia wanafunzi chuoni hapo ikiwemo karakana ya magari.

Amesema katika ziara hiyo amegundua chuo cha ufundi Arusha kina ujuzi na uwezo mkubwa wa teknolojia ikiwemo matumizi ya umeme jua kuendeshea mitambo hivyo wataona namna ya kufanya ushirikiano na chuo hicho Ili kutoa msaada kwa madereva visiwani humo.

Aidha amesema amefurahishwa na ushirikiano unaoendelea kati ya chuo cha ufundi Arusha (ATC), na kampuni ya usafirishaji ya Abnan Transport and Logistic Ltd ambapo chuo hicho kinafundisha walimu wa madereva kupitia kampuni hiyo.

“ Zanzibar tumekuwa na ongezeko la ajali za barabarani ambazo zimekuwa zikisababisha vifo na ulemavu kwa watu wengi, tunaamini ushirikiano huu unaoendelea na ule ambao tutaufanya hapo baadae utasaidia kuepusha ajali,” amesema.

Wakati huo huo, Naibu Waziri Badria amesema Serikali visiwani humo  imeanza mchakato wa kuondoa matumizi ya magari ya mafuta ndani ya Serikali yake na  kuanza kutumia magari ya umeme.

Amesema Serikali ya Zanzibar imeanza kubadilisha mfumo wa injinia za magari yake na kutumia umeme, na kwamba mfumo huo umeanzia kwenye magari ya umma ya usafirishaji na baadae wataendelea kwa magari ndani ya Serikali.

“ Chini ya Rais Dkt Hussein Alli Mwinyi, tumeanza kutumia magari ya umeme hasa kwa magari ya usafiri wa umma, na tutaendelea hadi kwenye magari ndani ya Serikali, naamini tutawatumia sana chuo hiki,” amesema.

Awali Mkuu wa Chuo cha ufundi Arusha, Profesa Mussa Chacha alisema chuo chake kimeingia ushirikiano na taasisi ya Abnan Transport and Logistic Limited ambapo walimu kutoka ATC wako visiwani humo wakiwafundisha walimu na madereva kozinya udereva.

Profesa Chacha amesema chuo cha ufundi ATC kimeshaanza utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050 Kwa kuanzisha vitengo vitakavyotumiwa na wanafunzi kujifunza ujuzi mbalimbali kutokana na bunifu wanazozifanya chuoni hapo.

“ Tumeshaanza utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050, hivi sasa tunajenga karakana ambayo itatumika kutengeneza vipuri vya magari na mitambo na hapa wanafunzi wetu ndio watakuwa wakitumia mitambo hiyo kuzalisha, pia jengo hilo litakuwa na karakana ya kutengeneza fenicha mbalimbali, tutakuwa tunatengeneza na kuuza,” amesema na kuongeza:

“ Pia tunakamilisha jengo la hospitali ambalo mbali ya kutoa huduma Kwa wagonjwa wanafunzi na wengine kutoka, nje pia wale wanafunzi wanaotengeneza bidhaa za hospital watatumia nafasi hiyo kujifunza badala ya kusubiri Hadi waendesha field,” .





Sajenti wa Polisi (SGT) Noela Pallangyo, kutoka Jeshi la Polisi Nchini Tanzania ambaye kwa sasa anahudumu katika Misheni ya Kulinda Amani nchini Sudan Kusini chini ya mwamvuli wa Umoja wa Mataifa nchini Sudan Kusini (UNMISS), ametunukiwa Barua ya Pongezi kwa kutambua utendaji wake wa kipekee, weledi na mchango wake katika utekelezaji wa majukumu ya kulinda amani.

Amebainisha kuwa baada ya kupokea pongezi hiyo, SGT Noela ameweka wazi kuwa tuzo hiyo ni heshima kwake binafsi Pamoja na nchi yake na Jeshi la Polisi Tanzania huku akiwashukuru viongozi wake na askari wenzake kwa ushirikiano uliomwezesha , kufikia hatua hiyo ya kutunukiwa Barua hiyo.

Barua hiyo ya pongezi imetolewa kwa kutambua huduma yake ya mfano kwa kazi yake chini ya mwamvuli huo wa Umoja wa Mataifa nchini Sudan Kusini (UNMISS), ambapo aliweza pia kutekeleza majukumu yake kama Afisa wa Rasilimali Watu (Personnel Officer) katika Makao Makuu ya Mission Headquarters – (MHQ).

Katika barua hiyo, kutoka Umoja huo (UNMISS) imeeleza kuwa SGT Noela amehudumu kwa umahiri, bidii na weledi wa hali ya juu, huku akionyesha kiwango kikubwa cha ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yake huku Misheni hiyo pia ikitambua mchango wake na umuhimu katika kufanikisha utekelezaji wa mamlaka ya (UNMISS) ya kulinda amani nchini Sudan Kusini.






Na Janeth Raphael - MichuziTv 

Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH) inaendelea kuthibitisha ubora wake kama moja ya vituo vinavyoongoza kutoa huduma za kibingwa barani Afrika, baada ya kufanikiwa kuwapatia matibabu ya upasuaji wa moyo watoto kutoka Nchini Burundi, ambao kwa sasa wanaendelea vizuri na wanatarajiwa kurejea nyumbani katika siku chache zijazo.

Mafanikio hayo yalidhihirika kupitia ziara ya Balozi wa Tanzania nchini Burundi, Gelasius Byakanwa, na Balozi wa Burundi nchini Tanzania, Leontine Nzeyimana, waliotembelea hospitalini hapo kuwajulia hali watoto hao pamoja na wazazi wao, huku wakishuhudia kwa karibu ubora wa huduma za kibingwa zinazotolewa na Hospitali ya Benjamin Mkapa.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, iliyofanyika leo  Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Benjamin Mkapa, Profesa Abel Makubi, amesema hospitali hiyo imeendelea kujijengea heshima ndani na nje ya Tanzania kwa kutoa huduma za kibingwa zinazowanufaisha wananchi wa Tanzania pamoja na mataifa jirani.

Profesa Makubi ameeleza kuwa mafanikio hayo yanatokana na uwekezaji mkubwa unaofanywa na Serikali katika sekta ya afya pamoja na juhudi za wataalamu wa hospitali hiyo.

Aidha, alikumbusha kuwa mwaka jana timu ya madaktari wa Hospitali ya Benjamin Mkapa ilifanya kambi maalum ya matibabu nchini Burundi, ambapo ilitoa huduma kwa wananchi zaidi ya 2,000 na kufanikisha upasuaji kwa wagonjwa zaidi ya 50, hatua iliyozidi kuimarisha ushirikiano wa afya kati ya Tanzania na Burundi.

"Tunafurahi kuwaona Mabalozi wa Tanzania na Burundi mmetenga muda kuja kuwajulia hali watoto hawa. Watoto wote watatu waliofanyiwa upasuaji wanaendelea vizuri na wanatarajiwa kurejea nyumbani katika siku chache zijazo," alisema Profesa Makubi.

Pia alimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kuwekeza katika miundombinu ya afya na kuziwezesha hospitali za nchini kutoa huduma za kibingwa zinazokidhi viwango vya kimataifa.

Kwa upande wake, Balozi wa Tanzania nchini Burundi, Gelasius Byakanwa, amesema ushirikiano kati ya Tanzania na Burundi umeendelea kuimarika, huku sekta ya afya ikiwa miongoni mwa maeneo yanayoonyesha mafanikio makubwa.

Ameeleza kuwa Serikali za nchi hizo mbili zilishirikiana kuhakikisha watoto hao pamoja na wazazi wao wanapatiwa nyaraka za kusafiria kwa haraka, ambapo pasi za kusafiria zilipatikana ndani ya saa 24 ili kurahisisha safari ya matibabu.

Kwa upande wake Balozi wa Burundi Nchini Tanzania Leontine Nzeyimana, ameishukuru SerikalI ya Tanzania kwa kuwapatia matibabu watoto hao toka Burundi na ameomba ushirikiano huo uzidi kuendelea.




Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt Mwigulu Nchemba amekagua maandalizi ya siku ya mashujaa yaliyofanyika katika uwanja wa Mashujaa uliopo Mji wa Serikali Mtumba Mkoa wa Dodoma.

Akizungumza mara maada ya kushuhudia majaribio ambayo yamefanywa na vikosi vya ulinzi na usalama amesema kuwa mpaka sasa mambo yanaenda vizuri na kupongeza maandalizi hayo.

"Nimekuja kujionea hatua ya maandalizi yanayoendelea kabla ya tukio letu kubwa na la kihistoria ambalo litafanyika tarehe 25/7/2026,, nikiri nimeridhishwa na maandalizi kufuatia taarifa ambayo tumepokea na kile ambacho tumejionea,,,.

Hapo awali Waziri wa Mambo ya Ndani kwa niaba ya Waziri wa Ulinzi Mhe,Patrobas Katambi akisoma taarifa ya maandalizi amesema katika ya siku ya mashujaa tayari vipo vikundi mbalilimbali kutoka katika vyombo vya ulinzi na usalama.

Ameongeza kwa kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu wa Vyombo vya ulinzi na Usalama Mhe.Dkt Samia Hassan kwa maelekezo yake mahususi kwa ajiri ya kuimarisha ulinzi na usalama wa nchi.

" Tunawahakikishia Wananchi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wako salama na kwa wageni wanaokuja kwa kufuata utaratibu nao wako salama,,.

Katika tukio hilo lilihudhuriwa na viongozi mbalimbali akiwemo Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe.Rosemary Senyamule na wakuu wa vyombo ulinzi na Usalama wa Mkoa huu.









Na Mwandishi Wetu, Tabora

Wananchi wa mikoa ya Tabora na Katavi wameanza kushuhudia matokeo ya Mradi Shirikishi wa Uhifadhi wa Misitu ya Miombo ya Nyanda Kame, huku shughuli za uhifadhi zikigeuka kuwa chanzo cha kipato, ajira na matumizi endelevu ya rasilimali za misitu.

Mafanikio hayo yamebainika wakati Kamati ya Wataalamu ya mradi ilipofanya ziara ya Julai 15 na 16, 2026 kukagua utekelezaji wa shughuli mbalimbali katika maeneo ya mradi na kujionea namna zinavyowanufaisha wananchi.

Akitoa taarifa ya maendeleo ya mradi mbele ya Katibu Tawala wa Mkoa wa Tabora kabla ya ziara hiyo, Kaimu Naibu Kamishna wa Uhifadhi, Dk. Zainabu Bungwa, alisema mradi umeanza kuleta mabadiliko yanayoonekana katika uhifadhi wa misitu na ustawi wa jamii kupitia uwekezaji kwenye shughuli za uzalishaji na maendeleo.

Alisema mradi umewezesha uanzishwaji wa vikundi vya wananchi vinavyojishughulisha na shughuli za kiuchumi, ujenzi wa miundombinu, ununuzi wa magari na pikipiki kwa ajili ya usimamizi wa rasilimali za misitu, ujenzi wa maghala ya kuhifadhi mbegu za miti, mashamba darasa ya kilimo mseto cha misitu, ufugaji wa nyuki, maeneo ya malisho ya mifugo pamoja na kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia.

“Tunaanza kuona matokeo chanya ya mradi katika maeneo mengi. Wananchi wanashiriki kikamilifu kwenye shughuli za uhifadhi huku wakiongeza kipato kupitia fursa zinazotokana na matumizi endelevu ya misitu,” alisema Dk. Bungwa.

Katibu Tawala wa Mkoa wa Tabora, John Gharuth Mboya, alisema mafanikio ya mradi yanapaswa kuambatana na uelewa wa pamoja wa viongozi wa mikoa na wilaya ili kuongeza ufanisi wa utekelezaji wake.

Alisema kuna umuhimu wa kuandaliwa taarifa ya kina itakayowasilishwa kwa Kamati za Ulinzi na Usalama za mikoa na wilaya husika ili kuzijengea uelewa kuhusu malengo, mafanikio na mchango wa mradi katika maendeleo ya wananchi.

Kwa upande wake, mwakilishi wa Katibu Tawala wa Mkoa wa Katavi ambaye pia ni Afisa Misitu wa Mkoa huo, Augustine Hildagadess, aliwataka wananchi kutenga maeneo rasmi ya malisho ya mifugo ili kupunguza migogoro ya matumizi ya ardhi na kuimarisha uhifadhi wa misitu.

Akizungumza baada ya kutembelea vijiji vya Mtakuja na Legezamwili wilayani Mlele, alisema wataalamu wa mradi wataendelea kushirikiana na vijiji kupanga matumizi bora ya ardhi yatakayolinda mazingira na wakati huo huo kukuza uzalishaji.

Katika ziara hiyo, Kamati ya Wataalamu iligawanyika katika makundi mawili. Kundi la kwanza lilikagua shughuli za mradi wilayani Sikonge, Kituo cha Ulinzi na Kituo cha Ufugaji Nyuki cha TFS Mlele pamoja na ofisi za viongozi wa Mkoa wa Katavi na Wilaya ya Mlele, huku kundi la pili likitembelea shughuli zinazotekelezwa katika wilaya za Urambo na Kaliua.

Mradi Shirikishi wa Uhifadhi wa Misitu ya Miombo ya Nyanda Kame unafadhiliwa na Mfuko wa Mazingira Duniani (GEF) kupitia Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO) kwa ushirikiano na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS).

Mradi huo wenye thamani ya dola za Marekani 6,785,882 unatekelezwa kuanzia mwaka 2023 hadi 2027 ukiwa na lengo la kurejesha takribani hekta 34,000 za misitu ya miombo iliyoharibiwa, kuboresha maisha ya wananchi wanaoizunguka misitu na kuimarisha usimamizi endelevu wa rasilimali za misitu.

Mbali na TFS na FAO, utekelezaji wa mradi unahusisha Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira), ICRAF, TARI, Wizara ya Maji, Wizara ya Mifugo, TAMISEMI pamoja na vikundi vya kijamii vinavyoshiriki katika shughuli za uhifadhi na maendeleo kwenye maeneo ya mradi.










 SUBIRA IMEKWISHA! 😱⚽

Fainali ya FIFA WORLD CUP 2026 inakuja na Oryx Energies tuko tayari kuitazama pamoja nawe! 

Tukutane Mbagala Zakhem

Jumapili | 19 July 2026 

Tunayo kwa ajili yako: 

🎉 Screen kubwa 

🎧 Live DJ & Burudani 

🍔 Vyakula na vinywaji 

💯 Hakuna kiingilio 


Wacha mpira unoge! Tujaze uwanja tucheke, tupige kelele na tushangilie pamoja 🇹🇿

Tag rafiki zako wa mpira hapa chini 👇

#OryxEnergies #FIFAWorldCup2026 #Fainali #MpiraNiFursa #Mbagala #Tanzania #WorldCupFinal



Na Hamis Dambaya - Stockholm

Balozi wa Tanzania nchini Sweden mheshimiwa Swahiba Mndeme amesema miongoni mwa kazi kubwa waliyonayo katika Ubalozi huo ni kutangaza vivutio vya utalii vya Tanzania katika nchi ya Sweden, Finland, Norway, Denmark, Iceland, Latvia, Lithuania, Estonia na Ukraine ili kuongeza idadi ya watalii kutoka nchi hizo kutembelea Tanzania.

Balozi Mndeme ametoa kauli hiyo alipokuwa akizungumza na maafisa kutoka Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro waliotembelea ofisi za ubalozi wa Tanzania nchini Sweden kushiriki programu mbalimbali ikiwemo siku ya tamasha la Kiswahili kwa lengo la kunadi vivutio vya utalii

“Maeneo ninayoyasimamia ya takriban nchi tisa ni ya kimkakati hivyo mimi na watumishi wenzangu katika ubalozi wetu, tunatumia fursa zilizopo katika nchi hizi kutangaza vivutio vyetu na ninaamini tukishirikiana kwa pamoja tutaibua soko jipya la utalii katika ukanda huu”,alisema balozi Mndeme.

Kwa upande wake Meneja mawasiliano na uhusiano kwa umma wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro Hamis Dambaya amesema Mamlaka ina mkakati wa kuibua mazao mapya ya utalii ikiwemo ya malikale, urithi utamaduni na kuendeleza mazao yaliyopo ili kuyaongezea thamani kwa wageni wanaotembelea hifadhi ya Ngorongoro.

“Tuna kampeni mbalimbali tunazoziendesha ikiwemo kuhamasisha watu duniani kurudi nyumbani Ngorongoro ili kupata ukweli kuhusu historia ya binadamu wa kale aliyepatikana katika eneo la Ngorongoro”,alisema bwana Dambaya.

Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro inatangaza shughuli zake za utalii nchini Sweden ambapo itashiriki katika tukio kubwa la maadhimisho ya siku ya kiswahili nchini humo.



Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba, leo Julai 17, 2026 amekagua na kupokea taarifa ya maandalizi ya Maadhimisho ya Siku ya Mashujaa yanayotarajiwa kufanyika Julai 25, 2026 katika Viwanja vya Mashujaa, Mtumba, jijini Dodoma.

Katika ukaguzi huo, Waziri Mkuu ameridhishwa na hatua zilizofikiwa na kuwataka wote wanaohusika kuendelea kukamilisha maandalizi yaliyobaki kwa wakati ili maadhimisho hayo yafanyike kwa utaratibu na hadhi inayostahili.

Maadhimisho hayo yataongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu.






Na Mwandishi Wetu
Kampuni ya MiXX imeendelea kuwazawadia wateja wake kupitia kampeni ya "Kombe la Dunia ya Ikiingia Tu... Golii!", inayowapa nafasi ya kujishindia zawadi kwa kufanya malipo ya huduma mbalimbali kupitia MiXX Super App.

Katika wiki ya nane ya kampeni hiyo, washindi sita walitangazwa, ambapo wanne walikabidhiwa fedha taslimu za shilingi milioni moja kila mmoja, huku washindi wawili wakijishindia vifaa vya kisasa vya Hisense.

Akizungumza katika hafla ya kukabidhi zawadi hizo jijini Dar es Salaam, Mkuu wa Kitengo cha Huduma na Malipo ya Kidijitali wa MiXX, Mshamma Mshamma, alisema kampeni hiyo imeendelea kuwafikia Watanzania wengi, huku jumla ya washindi 80 wakinufaika tangu ilipoanza.

Alisema washindi wamekuwa wakijishindia fedha taslimu pamoja na vifaa mbalimbali vinavyotolewa kwa ushirikiano na kampuni ya Hisense, jambo linaloonyesha dhamira ya MiXX ya kuwazawadia wateja wake waaminifu.

Mshamma alisema kampeni bado inaendelea, akibainisha kuwa mshindi wa mwisho ataondoka na zawadi kubwa ya shilingi milioni 50.

Aliwahimiza wananchi kuendelea kutumia MiXX Super App kufanya malipo ya huduma mbalimbali za kifedha ili kuongeza nafasi ya kushinda zawadi hizo.

"MiXX Super App ni zaidi ya programu ya malipo. Ni jukwaa linalorahisisha huduma za kifedha huku likiwapa watumiaji nafasi ya kujishindia zawadi mbalimbali," alisema Mshamma.

Mmoja wa washindi, Ibrahim Mandoa, mkazi wa Kinondoni, alisema ushindi wake umempa imani kuwa kampeni hiyo ni ya kweli na inawanufaisha watumiaji wa MiXX Super App.

"Nimefurahi sana kushinda na hii ni mara yangu ya kwanza kupata zawadi kama hii, na ninawahimiza Watanzania kuipakua na kuitumia MiXX Super App mara kwa mara kufanya malipo mbalimbali ili nao wapate nafasi ya kushinda," alisema Mandoa


Dar es Salaam, Julai 17, 2026

Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) umetangaza nafuu kwa waajiri wenye malimbikizo ya michango kwa kuwapatia fursa ya msamaha wa tozo zitokanazo na ucheleweshaji wa michango, huku ukiwataka kuchangamkia fursa hiyo ili kupunguza mzigo wa madeni, kuimarisha uzingatiaji wa sheria na kulinda haki za wafanyakazi.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mkuu wa NSSF, Bw. Masha Mshomba, alisema kuwa msamaha huo, ulioanza kutekelezwa tarehe 1 Juni 2026, utaendelea hadi 31 Desemba 2026.

Bw. Mshomba alieleza kuwa tangu kuanza kwa msamaha huo, waajiri wameonyesha mwitikio chanya ambapo hadi sasa zaidi ya waajiri 6,000 wamejitokeza kutumia fursa hiyo na Mfuko umekwishakusanya zaidi ya shilingi bilioni 46 za michango tangu kuanza kwa msamaha huo tarehe 1 Juni 2026.

“Tunawasihi waajiri wote kutumia fursa hii mapema. Fedha ambazo wangezilipa kama tozo wanaweza kuzielekeza katika shughuli za uzalishaji, upanuzi wa biashara, kuongeza tija na kuboresha ustawi wa wafanyakazi,” alisema Bw. Mshomba.

Alisema msamaha huo utaendelea hadi tarehe 31 Desemba 2026, ambapo waajiri watakaolipa malimbikizo yote ya michango ya msingi ifikapo tarehe 31 Agosti 2026 watanufaika na msamaha wa asilimia 100 ya tozo.

Alifafanua kuwa waajiri watakaokamilisha malipo yao kati ya Septemba na Oktoba 2026, watanufaika na msamaha wa asilimia 75, huku wale watakaolipa kati ya Novemba na Desemba 2026 wakipata msamaha wa asilimia 50.

Aidha, alisema waajiri ambao hawakuwa na malimbikizo ya michango hadi tarehe 31 Mei 2026 lakini walikuwa na tozo pekee, watanufaika na msamaha wa asilimia 100 endapo wataendelea kuwasilisha michango yao kwa wakati hadi mwezi Desemba 2026.

Bw. Mshomba alisema fursa hiyo imetolewa ili kuwapa waajiri nafasi ya kurekebisha hali ya ulipaji wa michango na kutumia fedha ambazo zingelipwa kama tozo katika shughuli za uzalishaji, kuongeza tija na kuboresha mazingira ya kazi.

“Fedha ambazo waajiri wamekuwa wakizilipa kwa ajili ya kufidia tozo zinaweza kuelekezwa katika kuboresha maeneo yao ya kazi, kuongeza tija na kuimarisha uzalishaji.

Ndiyo maana fursa hii imetolewa ili waajiri wanufaike,” alisema.

Alisema ulipaji wa michango kwa wakati ni muhimu kwa kuwa unamwezesha mfanyakazi kupata haki zake za hifadhi ya jamii wakati anapopata majanga mbalimbali ikiwemo kustaafu.

NSSF YAENDELEA KUIMARIKA

Katika hatua nyingine, Bw. Mshomba alisema NSSF imeendelea kuimarika katika kipindi cha Serikali ya Awamu ya Sita, ambapo thamani ya Mfuko imeongezeka kutoka shilingi trilioni 4.8 mwezi Machi 2021 hadi kufikia zaidi ya shilingi trilioni 11.6 Juni 2026.

Alisema ukuaji huo umechangiwa na ongezeko la wanachama na michango, uwekezaji wenye tija, mazingira mazuri ya uwekezaji pamoja na matumizi ya teknolojia katika kuboresha huduma.

Alieleza kuwa kupitia mifumo ya TEHAMA, waajiri na wanachama sasa wanaweza kufuatilia na kuwasilisha michango, kufuatilia madai ya mafao na kupata huduma mbalimbali bila kulazimika kufika katika ofisi za NSSF.

Kuhusu ulipaji wa mafao, Bw. Mshomba alisema Mfuko umeendelea kuboresha mifumo yake ambapo kwa sasa mafao mengi hulipwa ndani ya siku 20, tofauti na siku 60 zinazotakiwa kisheria.

“Lengo letu ni kuhakikisha mwanachama anapata stahiki zake kwa wakati. Endapo kuna ucheleweshaji mara nyingi chanzo huwa ni mwajiri kutowasilisha michango kwa wakati,” alisema.

UWEKEZAJI WENYE TIJA, SKIMU YA HIFADHI KUONGEZA WANUFAIKA

Akizungumzia uwekezaji, alisema NSSF inaendelea kutekeleza miradi ya kimkakati inayochangia ukuaji wa uchumi na kuongeza ajira, akitolea mfano Kiwanda cha Sukari cha Mkulazi ambacho kimeendelea kuongeza uzalishaji, kutoa ajira na kuwawezesha wakulima wanaokizunguka.

Kuhusu Skimu ya Hifadhi, Bw. Mshomba alisema mpango huo umewezesha wananchi waliojiajiri kujiunga na mfumo wa hifadhi ya jamii na kunufaika na mafao mbalimbali ikiwemo pensheni ya uzee, pensheni ya ulemavu, pensheni ya urithi, mafao ya uzazi, msaada wa mazishi pamoja na huduma za matibabu.

“Tunawahimiza waliojiajiri kujiunga kupitia Skimu ya Hifadhi kwa sababu mpango huu unabadilisha maisha yao na kuwapa uhakika wa kunufaika na mafao mbalimbali. Lengo letu ni kuhakikisha kila Mtanzania anakuwa Staa wa Mchezo katika kujilinda dhidi ya changamoto za maisha,” alisema Bw. Mshomba.

Alisema NSSF itaendelea kushirikiana na waajiri, wafanyakazi na wadau mbalimbali katika kuimarisha mfumo wa hifadhi ya jamii nchini na kuhakikisha unaleta manufaa kwa Watanzania wengi zaidi.

















Top News