Balozi wa Tanzania nchini Algeria, Mhe Mobhare Matinyi, akizungumza na vyombo vya habari vya Algeria wakati akitangaza kuwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imekubali mwaliko wa kuwa mgeni rasmi katika Maonesho ya Ufugaji wa Nyuki barani Afrika (Africa Bee Expo) yatakayofunguliwa jijini Algiers mnamo Septemba 3, 2026.
Bw. Fatah Benchouia, Mwenyekiti wa Maonesho ya Ufugaji wa Nyuki barani Afrika (Africa Bee Expo) ya mwaka 2026, akizungumza na vyombo vya habari vya Algeria wakati wa kuitangaza Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa mgeni rasmi.

TANZANIA imekubali mwaliko wa kuwa mgeni rasmi katika ufunguzi wa Maonesho ya Ufugaji wa Nyuki barani Afrika yatakayofanyika jijini Algiers, Algeria, tarehe 3-6 Septemba, 2026.


Akizunngumza na waandishi wa habari wa televisheni za Algeria kwenye Ubalozi wa Tanzania jijini Algiers, Balozi Mobhare Matinyi alisema Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji, ndiye atakayefungua maonesho hayo kwa niaba ya serikali.


Balozi Matinyi alisema Mhe. Waziri Dkt. Kijaji atakuja Algeria akiongoza ujumbe wa maafisa waandamizi na wataalamu wa serikali pamoja na wadau kutoka sekta binafsi ya ufugaji wa nyuki na utengenezaji wa bidhaa za nyuki nchini.


Balozi Matinyi alisema serikali inaipa sekta ya ufugaji wa nyuki umuhimu wa kipekee kwani inaajiri watu wapatao milioni mbili nchini na huingiza dola za Marekani milioni 77.5 (shilingi bilioni 205) kwa mwaka kutokana na mauzo ya asali katika nchi mbalimbali duniani.


Akinukuu takwimu za serikali, Balozi Matinyi alisema Tanzania hivi sasa ni ya pili kwa uzalishaji asali barani Afrika na ya kumi duniani na bado ikijipanga zaidi ina uwezo wa kufikisha mizinga ya nyuki takribani milioni 9.2 yenye uwezo wa kuzalisha tani 138,000 za asali na tani 9,200 za nta kwa mwaka.


Awali Mwenyekiti wa taasisi ya Algeria inayoandaa maonesho hayo, Fatah Benchouia, aliwaambia waandishi wa habari kwamba mbali ya uhusiano mzuri uliopo baina ya Algeria na Tanzania, lakini pia sababu kuu ya kuipa Tanzania heshima hii ni mafanikio yake katika sekta ya ufugaji wa nyuki ambapo kwa mwaka huzalisha tani 34,000 za asali kulinganisha na Algeria inayozalisha tani 7,300.


Bw. Benchouia aliambatana na Mwenyekiti wa Baraza la Kisayansi la taasisi inayoandaa maonesho hayo, Dkt. Abdelmadjid Bouchareb, pamoja na Rais na Afisa Mtendaji Mkuu wa Kituo cha Biashara cha Dunia hapa Algeria, Bw. Ahmed Tibaoaoui.


Maonesho hayo maarufu kwa jina la Africa Bee Expo 2026, yanafanyika kwa mara ya nne hapa Algeria na Tanzania inatarajia kuonesha mafanikio yake katika sekta hii na kujifunza kutoka kwa wafugaji na wazalishaji wa bidhaa za nyuki wa nchi zingine.


Imetolewa na Ubalozi wa Tanzania,
Algiers, Julai 20, 2026.

Katika kuhakikisha Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya linatoa huduma bora kwa wananchi kwa kutumia vifaa vya kielektroniki pamoja na mifumo mbalimbali ya kidigitali, wananchi na wadau Mkoani humo wapongezwa kwa kuendelea kushirikiana na Jeshi hilo katika kuzuia na kutokomeza uhalifu.

Hayo yamesemwa na Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Wilbert Siwa Julai 21, 2026 wakati akipokea msaada wa "Computer" iliyotolewa na Diwani wa Kata ya Ilemi kwa ajili ya kusaidia kazi za Polisi Jamii Wilaya ya Mbeya.

"Msaada huu umekuja wakati muafaka ambapo Jeshi la Polisi nchini limejikita katika matumizi ya mifumo mbalimbali ya kidigitali katika utendaji wake wa kazi, hivyo vifaa hivi vitasaidia kuongeza ufanisi na weledi katika utekelezaji wa majukumu mbalimbali" alisema Kaimu Kamanda Siwa.

Aidha, Kaimu Kamanda Siwa amesema kuwa elimu inayotolewa na Polisi na Wakaguzi Kata kwa makundi mbalimbali imesaidia wananchi kujua wajibu wao na kuzaa matunda ikiwemo kupungua kwa matukio ya uhalifu na kupata misaada mbalimbali ya vitendea kazi kama hivi vilivyotolewa na Waheshimiwa Madiwani wa Halmashauri ya Jiji la Mbeya.

Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Ilemi Mhe Baraka Zambi amesema kuwa, msaada huo umetolewa kutokana na ushirikiano mzuri uliopo kati ya Jeshi la Polisi na Wananchi katika maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Mbeya.

Aidha, Mhe Zambi amesema kuwa, kutokana na uwepo wa Polisi Jamii kwa sasa katika Kata ya Ilemi uhalifu umepungua ukilinganisha na hapo awali, vijana wameelimishwa na kubadilika na kubadili mienendo yao.

Naye, Diwani wa Kata ya Iwambi Mhe Gloria Mwamajemba maarufu Mchina amesema kuwa Polisi Kata wameleta matokeo chanya katika kuimarisha ulinzi na usalama kutokana na elimu inayotolewa pamoja na ushirikiano mkubwa uliopo kati ya Jeshi la Polisi na wananchi.

Kupitia falsafa ya Polisi Jamii, Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya limeendelea kushirikiana na wananchi kupitia utekelezaji wa miradi mbalimbali ya Polisi Jamii na kupelekea kupata mafanikio chanya ikiwemo kupungua kwa uhalifu.








TANZANIA inalenga kuongeza ushiriki wake katika soko la kimataifa la kaboni, huku kituo cha Taifa cha Ufuatiliaji wa Kaboni (NCMC) kikipewa jukumu la kuimarisha usimamizi, kuvutia uwekezaji wa kijani na kuongeza manufaa ya rasilimali za asili.

Katibu Mkuu katika Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Richard Muyungi, amesema Tanzania inapaswa kubadilika kutoka kuwa mshiriki wa kawaida katika biashara ya kaboni na kuwa miongoni mwa nchi zinazoongoza kwa kujenga mifumo thabiti itakayowezesha utekelezaji wa miradi ya kaboni yenye uadilifu wa hali ya juu.

Katibu Huyo Mkuu amesema hayo Julai 21 2016 jijini Dar es Salaam kwenye kikao  cha kwanza cha Bodi ya Wakurugenzi ya Kituo Cha Kaboni nchini kwa mwaka wa fedha 2026/2027.

Dkt. Muyungi amesema ukuaji wa uchumi wa kaboni duniani ni fursa muhimu kwa Tanzania kuongeza mapato ya Taifa sambamba na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

“Changamoto yetu sasa siyo kushiriki tu katika masoko ya kaboni, bali kuyaongoza,” alisema Dkt. Muyungi.

Amesema soko la kaboni duniani linaendelea kukua kwa kasi na sasa linakadiriwa kuwa na thamani ya zaidi ya dola za Marekani bilioni 107 kwa mwaka, huku Afrika ikiwa na uwezo wa kuzalisha takribani dola bilioni 6 kwa mwaka ifikapo 2030 endapo itatumia kikamilifu fursa zilizopo.

Dkt. Muyungi amesema Tanzania ina nafasi kubwa ya kunufaika kutokana na utajiri wa rasilimali zake ikiwemo misitu, maeneo oevu, mifumo ya ikolojia ya pwani na bahari, pamoja na fursa zilizopo katika nishati safi na kilimo kinachozingatia mabadiliko ya tabianchi.

Ameeleza kuwa hadi sasa Tanzania imesajili miradi 99 ya kaboni, huku zaidi ya mikopo ya kaboni milioni 13.4 ikiwa imetolewa. Hata hivyo, amesema mafanikio hayo bado hayajaakisi thamani halisi ya kiuchumi inayoweza kupatikana kupitia sekta hiyo.

“Mafanikio haya hayaoneshi manufaa yote tunayotarajia kutoka kwenye sekta ya kaboni. Tunahitaji kufanya zaidi kuhakikisha miradi inafikia hatua ya utekelezaji na kuanza kuleta thamani kwa Taifa na jamii zetu,” alisema.

Kutokana na hali hiyo, Dkt. Muyungi aliitaka bodi ya Kituo hicho kuimarisha mifumo ya usajili wa miradi ya kaboni, kuharakisha utekelezaji wa mifumo ya Ibara ya 6 ya Mkataba wa Paris kuhusu biashara ya kaboni na kuboresha mifumo ya Upimaji, Utoaji wa Taarifa na Uhakiki (MRV) ili kuongeza uwazi na kuimarisha imani ya wawekezaji.

Aidha, alisema Kituo hicho kinapaswa kuhakikisha manufaa yatokanayo na miradi ya kaboni yanagawanywa kwa haki, hasa kwa jamii zinazoshiriki katika uhifadhi wa mazingira, huku kikijenga uwezo wa wataalamu wa ndani katika mnyororo mzima wa thamani wa biashara ya kaboni.

“Tanzania lazima ijenge mfumo wa soko la kaboni unaovutia uwekezaji, unaolinda uadilifu wa mazingira na kuhakikisha wananchi wananufaika na fursa zinazotokana na sekta hii,” alisema.

Alisema usimamizi madhubuti wa sekta ya kaboni utachangia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kwa kuongeza mapato ya Serikali, kuvutia uwekezaji wa kijani, kuimarisha ustahimilivu wa jamii dhidi ya mabadiliko ya tabianchi na kuchochea maendeleo endelevu.

Katika hatua nyingine, Dkt. Muyungi aliitaka Menejimenti ya Kituo Cha Kaboni kukamilisha kwa haraka mifumo muhimu ya uendeshaji, ikiwemo kuboresha Mfumo wa Usajili wa Kaboni (Carbon Registry), kuwasilisha Mpango Mkakati wa Kituo na kuimarisha mifumo ya kitaasisi.

Pia aliitaka bodi ya Kituo hicho kuandaa taarifa ya kina kuhusu miradi yote ya kaboni iliyosajiliwa na ile iliyoanza utekelezaji kati ya Januari na Julai 2026, ikionesha hatua iliyofikiwa, kiwango cha uwekezaji na manufaa yanayotarajiwa kwa Taifa na wananchi.

Mwenyekiti wa Bodi ya Kituo cha Kaboni, Dkt. Albina Chuwa, ameahidi kutekeleza maelekezo hayo na kuongeza uelewa wa umma kuhusu biashara ya kaboni nchini, sambamba na kuimarisha utawala bora katika sekta hiyo.

Kituo cha Kaboni kilianzishwa kupitia marekebisho ya Sheria ya Usimamizi wa Mazingira kwa lengo la kuratibu ufuatiliaji wa kaboni, kuimarisha usimamizi wa masoko ya kaboni na kuiwezesha Tanzania kushiriki kikamilifu katika fursa za fedha za tabianchi duniani.








Na Janeth Raphael - MichuziTv 

Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dodoma, imeamuru Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), Melkisedeki Kaijage, aachiwe kwa dhamana kuanzia Julai 21, 2026, wakati uchunguzi wa tuhuma za uchochezi zinazomkabili ukiendelea.

Uamuzi huo umetolewa na Jaji Joachim Tiganga wakati wa usikilizwaji wa Shauri Na. 15653/2026.

Kaijage amekuwa akishikiliwa katika Kituo cha Polisi Chang’ombe akituhumiwa kuhamasisha maandamano yaliyojulikana kama “Sabasaba.”

Wakati wa usikilizwaji wa maombi hayo, upande wa Serikali uliieleza Mahakama kuwa haukuwa na pingamizi dhidi ya ombi la dhamana, na kwamba taratibu za kumwachia mshtakiwa zinaweza kuendelea kwa mujibu wa sheria.

Wakili wa Kaijage, Prosper Malangalila, alidai kuwa mteja wake alikaa mahabusu kwa siku 12 bila kufikishwa mahakamani, licha ya kosa analotuhumiwa kuwa la dhamana. Aliiomba Mahakama iamuru mteja wake aachiwe kwa dhamana, alipwe fidia kwa kuzuiliwa kwa muda huo, na Serikali ilipe gharama za maombi hayo.

Baada ya kusikiliza hoja za pande zote, Mahakama ilikubali ombi la dhamana na kuamuru Kaijage aachiwe kwa masharti ya dhamana. Hata hivyo, ilikataa ombi la kulipwa fidia kwa kipindi alichokuwa mahabusu.

Mahakama imeeleza kuwa baada ya uchunguzi kukamilika, Kaijage atafikishwa mahakamani kujibu rasmi tuhuma zinazomkabili.

Akizungumza nje ya Mahakama, Wakili Prosper Malangalila amesema upande wake umepokea uamuzi huo na utaendelea kufuatilia hatua zinazofuata za kisheria katika shauri hilo.





Njedengwa - Dodoma 📍

SERIKALI inaendelea na utekelezaji wa mkakati wake wa kuongeza tija katika kilimo baada ya kusambaza pampu za Umwagiliaji kwa vikundi vya wakulima na kuchimba visima 390 katika mikoa 15, hatua inayotarajiwa kuwawezesha wakulima kulima mwaka mzima na kuongeza uzalishaji wa mazao.

Hatua hiyo itawanufaisha wakulima 15,022 kupitia vikundi 769, huku eneo la ekari 13,518.75 likitarajiwa kuingia kwenye kilimo cha umwagiliaji na kupunguza utegemezi wa mvua.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma, Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji (NIRC), Raymond Mndolwa, alisema pamoja na Tume kuendelea na ujenzi wa miradi ya Umwagiliaji na ile ya kimkakati pia inaendelea kutekeleza kwa vitendo mkakati wake wa kuongeza tija katika kilimo kwa kusambaza pampu za Umwagiliaji kwa vikundi vya wakulima na kuchimba visima 390 katika mikoa 15.

Hatua hiyo inatarajiwa kuwawezesha wakulima kulima mwaka mzima na kuongeza uzalishaji wa mazao.

Alisema, mpango huo unatekeleza maelekezo ya Serikali ya kuwawezesha wakulima wenye mashamba madogo kujikwamua kiuchumi hususani wanawake na vijana kwa kupata uhakika wa maji.

"Tumeelekezwa kutafuta njia zitakazowawezesha wananchi wa kipato cha chini kujiongezea kipato. Ndiyo maana pamoja na miradi mikubwa ya Umwagiliaji, tumeanza uchimbaji wa visima na ugawaji wa pampu kwa wakulima wadogo," alisema.

Alisema pampu hizo ni maalumu kwa wakulima wanaolima karibu na mito na maziwa ili kuwasaidia kufanya kilimo kinachohifadhi mazingira na kuongeza uzalishaji.

Mndolwa alisema kati ya pampu 2,000 zilizonunuliwa na Serikali, pampu 1,000 tayari zimepokelewa na kupelekwa katika mikoa ya Mwanza, Mara, Kagera, Kigoma, Simiyu, Geita na Katavi kwa ajili ya kuanza kutumika.

Alisema pampu hizo zitagawiwa kwa vikundi 769 vya wakulima na kunufaisha wanawake 6,335 na wanaume 8,702, hivyo kufikisha jumla ya wanufaika 15,022.

"Pampu hizi zitawasaidia wakulima kuondokana na utegemezi wa mvua na kuwawezesha kulima misimu yote ya mwaka, jambo litakaloongeza uzalishaji na kipato chao," alisema.

Mndolwa alisema hadi sasa Tume imechimba visima 390 katika mikoa 15, ambapo Dodoma inaongoza kwa visima 93, ikifuatiwa na Manyara na Tabora zenye visima 44 kila mmoja, Geita 42, Singida 32, Njombe 30, Tanga 22, Iringa 20, Mara na Morogoro visima 17 kila mmoja.

Alitaja mikoa mingine iliyonufaika ni Pwani na Arusha zenye visima 10 kila mmoja, Mtwara nane, Mbeya saba na Ruvuma visima vitano.

Alisema Serikali pia imeanza ununuzi wa pampu 500 kwa ajili ya visima hivyo, ambapo pampu 100 tayari zimepokelewa, nyingine 100 ziko njiani kutoka kwa mtengenezaji na pampu 300 zipo katika hatua za manunuzi.

Mbali na pampu hizo, alisema Serikali inatarajia kupokea pampu nyingine 1,000 zinazotumia nishati ya jua ambazo zitasambazwa katika maeneo yenye changamoto ya upatikanaji wa umeme ili kuongeza wigo wa kilimo cha umwagiliaji.

Alifafanua kuwa visima vinachimbwa kwenye mashamba ya wakulima baada ya kuunganishwa katika vikundi, lakini hubaki kuwa mali ya umma ili wanakikundi wote wanufaike kwa usawa na kuhakikisha huduma hiyo inadumu.

Aidha, alisema vikundi vyote vinavyonufaika husajiliwa kwa mujibu wa sheria ili kurahisisha usimamizi wa miradi hiyo pamoja na ukusanyaji wa mapato ya Serikali.

Mndolwa alisema utekelezaji wa mradi huo unatarajiwa pia kutoa ajira kwa zaidi ya vijana 4,000 watakaoshiriki katika ufungaji, uendeshaji na usimamizi wa mifumo ya Umwagiliaji, huku akisisitiza kuwa lengo la Serikali ni kuhakikisha Umwagiliaji unakuwa chachu ya mapinduzi ya kilimo, usalama wa chakula na ukuaji wa uchumi wa wananchi.



Dar es Salaam

‎Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Prof. Palamagamba Kabudi amesisitiza umuhimu wa kuhakikisha miradi inayotekelezwa kupitia mradi wa Uboreshaji Jiji la Dar es Salaam (DMDP) inazingatia ubora, kasi ya utekelezaji na matumizi sahihi ya fedha za umma.

‎Prof. Kabudi amesema kuwa fedha zinazotumika katika mradi huo ni mkopo ambao serikali italipa, hivyo ni wajibu wa kila anayehusika na utekelezaji kuhakikisha fedha hizo zinatumika kwa ufanisi na kuleta thamani halisi kwa watanzania.

‎Pia Prof. Kabudi ameridhishwa na maendeleo ya ujenzi wa jengo la ofisi ya TARURA wilaya ya Ubungo unaoendelea chini ya mradi huo huku akiwapongeza wakandarasi, washauri elekezi na watendaji wote wanaosimamia utekelezaji wa mradi huo.

‎‎Aidha, amewataka washauri elekezi kusimamia kwa karibu utekelezaji wa miradi ili kuhakikisha kazi zote zinafanyika kwa kuzingatia viwango vinavyotakiwa na thamani ya fedha inaonekana katika kila hatua ya utekelezaji.

‎Akikagua ujenzi wa barabara ya Kizota- Changanyikeni iliyopo wilayani Kinondoni,  Prof. Kabudi amesisitiza umuhimu wa kujenga mifereji ya maji sambamba na barabara, akieleza kuwa kutokuwepo kwa mifereji husababisha maji ya mvua kuharibu barabara mapema na kusababisha hasara kwa serikali.

‎‎Sambamba na hilo amewataka wananchi kutoa ushirikiano na kuepuka kutupa taka hovyo katika mifereji na madaraja. 

‎‎Amehitimisha kwa kuwapongeza wataalamu kutoka Manispaa ya Kinondoni, Ofisi ya Mkoa, TARURA na wote wanaoshiriki katika utekelezaji wa mradi huo na kuwataka kuendelea kufanya kazi kwa bidii, uadilifu na weledi ili miradi hiyo ikamilike kwa ubora uliokusudiwa.

‎‎Wakizungumza kwa nyakati tofauti wananchi  wametoa shukrani zao za dhati kwa serikali kwa ujenzi wa barabara hiyo wakisema imewapandisha hadhi na heshima.














Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiagana na Viongozi mbalimbali kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) Jijini Dar es Salaam kabla ya kuondoka nchini, kuelekea Accra, Ghana kushiriki katika Mkutano Mkuu Maalum wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika (AU) kuhusu afya, utakaofanyika tarehe 22 Julai, 2026 jijini Accra.



 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiondoka nchini kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) Jijini Dar es Salaam tarehe 21 Julai, 2026 kuelekea Accra, Ghana ambapo atashiriki katika Mkutano Mkuu Maalum wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika (AU) kuhusu afya, utakaofanyika tarehe 22 Julai, 2026 jijini Accra.




Na Mwandishi Wetu, Bahi

Wanawake wa Wilaya ya Bahi mkoani Dodoma wamehimizwa kupaza sauti dhidi ya vitendo vya ukatili wa kijinsia vinavyoendelea kuathiri wanawake, watoto na maendeleo ya jamii.

Wito huo umetolewa katika mdahalo ulioandaliwa na Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo la Ujerumani (GIZ), ukiwaleta pamoja wanawake na viongozi mbalimbali kujadili namna ya kukabiliana na ukatili wa kijinsia.

Akifungua mdahalo huo, Mkurugenzi wa TAMWA, Dk. Rose Reuben amesema ukatili wa kijinsia una sura nyingi na huathiri watu kwa namna tofauti.

"Kuna ukatili wa aina nyingi na kila mmoja amepitia kwa aina yake. Tupo hapa kujifunza ili kupata maarifa zaidi na kwa pamoja tuendelee kupaza sauti zetu," alisema.

Afisa Elimu Mkoa wa Dodoma, Kumburusa Elias, alisema jamii bado inakabiliwa na changamoto ya kutokuchukua hatua dhidi ya vitendo vya ukatili, hata pale vinapotokea ndani ya familia.

"Ukatili wa wanawake upo na tunauona, lakini kwa bahati mbaya sisi wanawake wenyewe hatuchukui hatua kupaza sauti zetu. Utamkuta mama anaungana na baba kuhakikisha mtoto mlemavu haendi shule kwa kuogopa aibu," alisema.

Aliongeza kuwa baadhi ya watoto wa kike bado wananyimwa haki ya elimu kwa shinikizo la wazazi wanaotaka waolewe mapema.

"Usikubali mtoto wako wa kike akatishwe elimu na baba kwa kigezo cha kuolewa. Tafuta namna yoyote kwa siri utoe taarifa zitakazomsaidia kupata haki yake," alisisitiza.

Naye Afisa Maendeleo Mkoa wa Dodoma, Neema, aliwataka wanawake kutumia fursa za vikundi vya kiuchumi kujiondoa kwenye utegemezi unaochochea ukatili wa kiuchumi.

"Kama mradi wa TAMWA unavyosema Sauti Zetu, sisi wamama tupaze sauti zetu kwa pamoja kukemea ukatili wa aina zote. Tunalo jukumu la kutumia fursa za vikundi kujikwamua kiuchumi na kuwa mabalozi wa kupinga ukatili," alisema.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wanawake, Janeth Nyamayahasi, alisema baadhi ya vitendo vya ukatili vimezoeleka kiasi cha kutotambuliwa kama ukatili.

"Wakati mwingine sisi wenyewe tunafanya ukatili bila kujua. Tunao watoto wa kike wanaolazimishwa kwenda kufanya kazi mijini ili kusaidia familia, huku wanawake wakikosa haki ya kuamua matumizi ya mazao wanayoyalima. Huu pia ni ukatili," alisema.

Akizungumza kuhusu hatua za kisheria zinazopatikana kwa wahanga, Mrakibu wa Polisi kutoka Dawati la Jinsia na Watoto Mkoa wa Dodoma, Christa Yasinta Kayombo, alisema madawati hayo yameanzishwa katika vituo vya polisi ili kusaidia wahanga kwa usiri na weledi.

"Dawati la Jinsia na Watoto ni ofisi maalumu iliyoanzishwa katika kila kituo cha polisi. Tunafanya kazi kwa usiri na weledi kusaidia wahanga wa ukatili wa kijinsia. Jiamini kabisa unapotoa taarifa, itabaki kuwa siri," alisema.

Mrakibu Kayombo alisema ukatili ni kosa la kisheria na haukubaliki kwa misingi ya dini wala utu.

"Ukatili kwa imani zote ni dhambi, penye ukatili hakuna upendo. Vitendo vya ukatili vinakiuka sheria na vinapaswa kukemewa na kila mwanajamii," alisema.

Pia aliitaka jamii kuacha kuficha vitendo vya ukeketaji, ulawiti na aina nyingine za ukatili vinavyofanywa dhidi ya watoto wa kike na wa kiume.

Mdahalo huo umefanyika chini ya mradi wa Sauti Zetu unaotekelezwa na TAMWA kwa kushirikiana na GIZ, ukiwa na lengo la kuongeza uelewa wa jamii kuhusu haki za wanawake na watoto na kuhamasisha wananchi kushiriki katika kutokomeza ukatili wa kijinsia.


📍Wamwangukia DPP amuachie Lissu


Na Mashaka Mhando, Tanga

VIONGOZI wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) ngazi ya majimbo mkoani Tanga, wamemtaka Makamu Mwenyekiti wa chama hicho (Bara), John Heche, kujiuzulu au kukaa pembeni kupisha uchunguzi kufuatia tuhuma za ubadhirifu wa fedha zinazomkabili.

Sambamba na shinikizo hilo la ndani ya chama, viongozi hao wameiomba Serikali kupitia Mwanasheria Mkuu na Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP), kufuta kesi ya uhaini inayomkabili Mwenyekiti wao wa Taifa, Tundu Lissu, na kumuachia huru.

Msimamo huo umetolewa Julai 20 na Katibu wa CHADEMA Wilaya ya Handeni Mjini, Kombo Mohamed Maturu alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari akiwa ameambatana na viongozi wa majimbo mbalimbali na wanachama.


Taharuki na Tuhuma Dhidi ya Heche

Katibu huyo alieleza kuwa wamelazimika kuita waandishi kutokana na taharuki kubwa inayoendelea ndani ya chama chao inayotokana na misigano kati ya viongozi na wanachama, jambo linalokosesha chama afya. Alifichua kuwa awali walipanga kufanya maandamano makubwa kufikisha kilio chao.

"Kwanini Heche asizijibu hizi tuhuma au asitupishe akae pembeni ili tuchunguze tuhuma zake? Badala yake anakuja kujibu kwa kuwasema vibaya watu ambao tunawategemea kama wawakilishi... chama kipo chini kwa wanachama," alisema Matumla.

Maturu alimshutumu Heche kwa kutumia lugha isiyo ya kiungwana dhidi ya wawakilishi wao kwa kuwaita ‘mbwa’ badala ya kujibu hoja zinazoelekezwa kwake, huku akimtaka aache kugombana na Mjumbe wa Kamati Kuu, Godbless Lema.

"Haya ni masikitiko yetu makubwa. Makamu Mwenyekiti wetu anatuhumiwa kufanya ubadhirifu halafu anajifanya mbabe. Tunataka ajibu tuhuma hizi au ajiuzulu mara moja. Hiki si chama cha mtu binafsi, ni taasisi ya watu. Tunampenda sana Heche, lakini atupishe hata wiki moja tufanye uchunguzi," alisisitiza.


Madai ya Meli ya Mafuta na Wito kwa Msajili

Katika madai mazito zaidi, Maturu alidai kuwa chama hicho kimekosa ujasiri wa kulalamikia upandaji wa bei za mafuta nchini kutokana na madai kuwa kiongozi wao wa juu anashirikiana na wafanyabiashara wa mafuta. Alihusisha hilo na tukio la hivi karibuni la kukamatwa kwa meli ya mafuta huko Yemen iliyokuwa inapeperusha bendera ya Tanzania.

Kutokana na mzozo huo, viongozi hao wamemwomba Katibu Mkuu wa CHADEMA, John Mnyika, kuunda tume ya kuchunguza madai hayo na asifanye mzaha na kauli za viongozi kuitana 'mbwa'. Pia, wamemtaka Msajili wa Vyama vya Siasa nchini kuingilia kati mgogoro huo ili kunusuru chama.

Kilio kwa Tundu Lissu

Kuhusu hali ya kisiasa, Maturu alisema licha ya kutokubaliana na ushindi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), kilio chao kikubwa kwa sasa ni kutaka Lissu aachiwe huru.

"Tunaomba Serikali iwe na huruma. Hii kesi ya Lissu ni ya kisiasa, haiwezekani mwaka wa pili sasa aendelee kushikiliwa kizuizini. Nchi inaingia kwenye migogoro na mataifa ya Ulaya na tunazuiwa misaada. Tunamuomba DPP aifute hii kesi, hakuna faida kuendelea kumshikilia," aliomba Maturu.


Msimamo wa BAVICHA na BAWACHA

Mwenyekiti wa Baraza la Vijana CHADEMA (BAVICHA) Jimbo la Lushoto, Mambo Nassor Mkuya, aliunga mkono uamuzi wa viongozi hao wa Tanga wa kumtaka Heche apishe uchunguzi kwa kuwa chama ni cha wanachama na tuhuma hizo haziwezi kuachwa zipite. Mkuya alisisitiza kuwa kama Lissu angekuwepo, ubadhirifu huo usingetokea.

Naye Katibu wa CHADEMA Wilaya ya Lushoto ambaye pia ni Mwenyekiti wa BAWACHA wilayani humo, Jerida Ramadhani Mosha, alisema kuendelea kubaki ofisini kwa Heche kunaleta mgogoro. Aidha, alimuomba DPP "kuvaa viatu vya Lissu" na kujiona kama sehemu ya familia inayopata uchungu wa kiongozi huyo kukaa ndani kwa miaka miwili.






Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Afrika inapaswa kutumia mabadiliko yanayoendelea katika siasa, uchumi na usalama duniani kama fursa ya kuharakisha maendeleo yake.

Amesema inapaswa kufanya hivyo kwa kuimarisha uongozi wa kimkakati, kuongeza thamani ya rasilimali zake na kujenga taasisi imara zitakazolinda maslahi ya wananchi wake na kuharakisha maendeleo ya Bara la Afrika.

"Afrika isiendelee kuwa uwanja wa ushindani wa mataifa makubwa. Tunapaswa kutumia nafasi yetu ya kimkakati, rasilimali tulizonazo na nguvu ya watu wetu kujiletea maendeleo yenye manufaa kwa wananchi wetu," amesema.

Waziri Mkuu alisema hayo leo (Jumanne, Julai 21, 2026) alipokuwa Mzungumzaji Mkuu katika Mkutano wa Pili wa Wahitimu wa Chuo cha Taifa cha Ulinzi Tanzania (National Defence College – Tanzania) uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere (JNICC), jijini Dar es Salaam.

Alisema dunia inaendelea kushuhudia mabadiliko makubwa ya kisiasa, kiuchumi na kiusalama yanayochochewa na ushindani wa mataifa makubwa, maendeleo ya teknolojia, mabadiliko ya nishati na ushindani wa rasilimali muhimu, hali inayozitaka nchi za Afrika kuwa na viongozi wenye uwezo wa kufanya maamuzi ya kimkakati kwa manufaa ya Bara.

Alisisitiza Afrika ina takribani asilimia 30 ya madini muhimu yanayohitajika katika mapinduzi ya teknolojia na nishati safi duniani, hivyo Bara hilo linapaswa kutumia nafasi hiyo kujenga uchumi imara kupitia kuongeza thamani ya rasilimali zake badala ya kuendelea kuuza malighafi na kutegemea mataifa mengine.


"Afrika lazima iache kuwa uwanja wa ushindani wa mataifa makubwa. Tunapaswa kujenga uwezo wa kuongeza thamani ya rasilimali zetu, kuimarisha biashara ndani ya Bara na kutumia fursa zilizopo kujenga uchumi shindani na endelevu," alisisitiza.

Aidha, Waziri Mkuu amesema viongozi wa Afrika wanapaswa kujenga taasisi zenye uwezo wa kusimamia maendeleo, kulinda maslahi ya wananchi na kuhakikisha rasilimali za Bara zinatumika kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.

Akizungumzia hali ya usalama duniani, Waziri Mkuu alisema migogoro ya kimataifa imeendelea kuathiri uchumi wa Afrika kupitia kupanda kwa gharama za nishati, usafirishaji, bidhaa na huduma, hali inayosisitiza umuhimu wa nchi za Afrika kujenga uchumi unaostahimili misukosuko ya nje, kuimarisha biashara baina ya nchi za Afrika na kuongeza ushirikiano wa kikanda.

Alisema changamoto hizo zinapaswa kuwa chachu ya Afrika kuwekeza zaidi katika viwanda vinavyoongeza thamani ya malighafi, teknolojia, utafiti na ubunifu ili kujenga uchumi imara na unaojitegemea.

Dkt Mwigulu pia aliwataka washiriki wa mkutano huo, ambao ni viongozi waandamizi kutoka sekta mbalimbali, kutumia jukwaa hilo kujadili na kutoa mapendekezo yatakayosaidia Afrika kubadili changamoto za kisiasa, kiuchumi na kiusalama kuwa fursa za maendeleo endelevu.

Awali, Mkuu wa Chuo cha Taifa cha Ulinzi Tanzania, Balozi Meja Jenerali Wilbert Ibuge, alisema mkutano huo unalenga kuwakutanisha wahitimu wa chuo hicho ili kubadilishana uzoefu, kuimarisha mtandao wa viongozi wa kimkakati na kujadili masuala muhimu yanayohusu siasa, uchumi, uongozi na usalama kwa maendeleo ya Afrika.

Naye, Kansela wa Chuo cha Taifa cha Ulinzi Tanzania, Dkt. Abdulhamid Mzee, alisema mkutano huo ni jukwaa muhimu la kitaaluma linalowakutanisha wahitimu, wataalamu na viongozi mbalimbali kwa ajili ya kujadili changamoto na fursa zinazolikabili Bara la Afrika katika mazingira ya sasa ya dunia.

Baada ya mzungumzaji mkuu kuwasilisha mada yake, mkutano uliendelea kwa mjadala wa kitaalamu kuhusu mwenendo wa siasa, uongozi, uchumi na usalama katika karne ya 21 pamoja na athari zake kwa maendeleo ya Afrika, uliowashirikisha wataalamu na viongozi mbalimbali akiwemo Profesa Rwekaza Mukandala, Balozi Ombeni Sefue, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda, Kamanda wa Jeshi la Kenya na mhitimu wa Chuo cha Taifa cha Ulinzi Tanzania, Luteni Jenerali David Kipkemboi Ketter, na Profesa Palamagamba Kabudi, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu). 








Top News