MRATIBU wa Jukwaa la Kimataifa la Biashara na Uwekezaji la Kilimo na HortiLogistica Africa, Loveness Adolf, amewakaribisha wakulima, wafanyabiashara, wawekezaji na wadau wengine wa sekta ya kilimo kujisajili mapema kushiriki HortiLogistica Africa 2026, itakayofanyika Novemba 8 hadi 10, 2026 katika Hoteli ya Ngurdoto, Arusha.

Amesema jukwaa hilo lenye kaulimbiu “Kuunganisha Masoko, Kukuza Ustawi” linatarajiwa kuwa na zaidi ya waonyeshaji 500 na kuvutia wageni kati ya 10,000 na 12,000, likilenga kuwaunganisha wadau mbalimbali wa sekta ya kilimo na biashara.

Loveness amesema tukio hilo litatoa nafasi kwa washiriki kuonyesha bidhaa na huduma zao, kujenga mahusiano ya kibiashara na kutafuta fursa mpya katika masoko ya ndani na kimataifa.
Akizungumzia nafasi ya kilimo hai katika uchumi, Afisa Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Kilimo Hai Tanzania (TOAM), Bakari Mongo, amesema kilimo hicho kina uwezo wa kuongeza uzalishaji, thamani ya mazao na ushindani wa bidhaa za Tanzania katika masoko mbalimbali.

Amesema Tanzania ina fursa kubwa katika uzalishaji wa viungo, mazao ya asili na bidhaa nyingine zinazoweza kuongezewa thamani kupitia uchakataji, hivyo wakulima na wajasiriamali wanapaswa kutumia fursa hizo kukuza biashara zao.

Mongo amesema ushirikiano kati ya wakulima, vikundi vya wazalishaji, wasindikaji, wafanyabiashara na wadau wa uwekezaji ni muhimu katika kuhakikisha bidhaa za kilimo hai zinafikia masoko yenye tija.

Wakati huo huo Loveness amesema Jukwaa hilo litakuwa na shughuli mbalimbali zitakazowapa washiriki nafasi ya kujifunza, kubadilishana uzoefu na kufurahia mazingira ya Arusha wakati wa mkutano huo.

Amesema miongoni mwa shughuli zitakazofanyika ni camping, wellness ikiwemo huduma za massage, food fun run kutoka Mbuga kuelekea Arusha National Park, pamoja na programu ya ‘African Invite’ itakayolenga kuonyesha vyakula, utamaduni na burudani mbalimbali za Afrika.

Amesema pia kutakuwa na maonesho yanayoangazia mwelekeo wa sekta ya kilimo na utalii kwa miaka ijayo, yakiwemo maendeleo ya uzalishaji na uuzaji wa mazao kama parachichi, ili kuwawezesha washiriki kupata taswira ya fursa zinazoweza kujitokeza katika sekta hizo.

Kilimo hai chatajwa kuwa fursa ya kukuza biashara na masoko ya kimataifa
Mwanachama wa Taasisi Mwavuli ya Kilimo Hai Tanzania (TOAM), Charles Bupamba, amesema wadau wa sekta ya kilimo wanatakiwa kutumia fursa zinazotokana na kilimo hai na kilimo ikolojia kuongeza uzalishaji wa bidhaa bora, salama na zenye ushindani katika masoko ya ndani na kimataifa. 

Bupamba amesema kilimo hai na kilimo ikolojia si jambo la kupuuzwa, kwani Tanzania ina wakulima na wazalishaji wanaojihusisha na uzalishaji wa bidhaa mbalimbali, ikiwamo viungo, mazao ya asili na bidhaa nyingine ambazo zinaweza kusindikwa, kuongezwa thamani na kuuzwa katika masoko mbalimbali.

Amesema kilimo hai na kilimo ikolojia ni miongoni mwa suluhisho muhimu kwa maendeleo ya sekta ya kilimo, huku kikitoa fursa kwa wakulima, vikundi vya wazalishaji, wasindikaji, biashara ndogo na za kati pamoja na vijana kuongeza thamani ya mazao na kukuza biashara zao.

Amesisitiza kuwa ushirikiano wa wadau ni muhimu katika kukabiliana na changamoto zinazowakabili wakulima, wazalishaji na wafanyabiashara, akieleza kuwa majukwaa ya kimataifa yanatoa fursa kwa wadau kuonyesha bidhaa zao, kukutana na wanunuzi kutoka maeneo mbalimbali duniani, kujenga ushirikiano na wataalamu, kubadilishana uzoefu na maarifa, pamoja na kutafuta masoko mapya. Amesema pia majukwaa hayo yanawezesha wadau kujifunza teknolojia mpya katika kilimo, usindikaji na mifumo ya mnyororo wa thamani, hivyo kuongeza tija na ushindani wa bidhaa za Tanzania.

Na Janeth Raphael - MichuziTv

Bodi ya Wataalamu wa Ununuzi na Ugavi (PSPTB) imewataka wataalamu wote waliosajiliwa ambao hawajalipa ada zao za mwaka kukamilisha malipo ya madeni yote ndani ya siku 30, ikionya kuwa watakaoshindwa kutekeleza agizo hilo wanaweza kuchukuliwa hatua za kinidhamu na kisheria, ikiwemo kufutiwa usajili na majina yao kuchapishwa rasmi.

Mkurugenzi Mtendaji wa PSPTB, Godfred Mbanyi, ametoa kauli hiyo leo jijini Dodoma wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu utekelezaji wa wajibu wa wataalamu waliosajiliwa na Bodi. Amesema hatua hizo zinalenga kuhakikisha wataalamu wanatimiza wajibu wao kwa mujibu wa sheria na kanuni zinazosimamia taaluma ya ununuzi na ugavi nchini.

PSPTB ni taasisi ya Serikali iliyo chini ya Wizara ya Fedha, iliyoanzishwa kwa mujibu wa Sheria ya Bodi ya Wataalamu wa Ununuzi na Ugavi, Sura ya 179 ya Sheria za Tanzania. Bodi ina jukumu la kusimamia na kudhibiti viwango, mwenendo na maadili ya taaluma hiyo, huku ikiwa na mamlaka ya kusajili watu wanaokidhi vigezo na kuwapa uhalali wa kufanya kazi za kitaaluma katika eneo hilo.

Bodi imekumbusha kuwa ulipaji wa ada ya mwaka ni wajibu wa kisheria kwa kila mtaalamu aliyesajiliwa, kwa mujibu wa kanuni zake, ikiwemo Tangazo la Serikali Na. 364 la mwaka 2009. Mtaalamu anayeshindwa kulipa ada hiyo kwa kipindi cha miezi 24 mfululizo anaweza kupoteza hadhi ya usajili na jina lake kuondolewa kwenye daftari rasmi la PSPTB.

Aidha, PSPTB imeonya kuwa mtu anayeendelea kufanya kazi, kujitambulisha au kujihusisha na taaluma ya ununuzi na ugavi bila kuwa amesajiliwa na Bodi anafanya kosa la jinai na anaweza kuchukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria. Kwa mujibu wa Kifungu cha 46(2) na (3) cha Sheria ya PSPTB, Bodi ina mamlaka ya kuchukua hatua za kisheria na kinidhamu dhidi ya wanaokiuka masharti hayo.

Kwa hatua hiyo, PSPTB imewataka wataalamu wote wenye madeni ya ada ya mwaka kuhakikisha wamelipa madeni yao yote ndani ya siku 30 kuanzia tarehe ya tangazo hilo. Bodi imesisitiza kuwa watakaokaidi watachukuliwa hatua, ikiwemo kufutiwa usajili, kuchapishwa kwa majina yao na, pale inapobidi, kufunguliwa mashitaka kwa mujibu wa sheria iliyoanzisha Bodi.



*Pia atoa maelekezo kwa TANROAD,Wakandarasi, wamiliki wa majengo 


Na Said Mwishehe,Michuzi TV

MKUU wa Wilaya ya Ilala jijini Dar es Salaam Edward Mpogolo ametoa maelekezo kwa wafanyabishara katika maeneo ya Kariakoo katika kila meza tatu kunakuwa na chombo cha kuhifadhia taka huku pia wakandarasi nao wakitakiwa kuweka vyombo vikubwa Vya taka katika mitaa.

Mpogolo ametoa maelekezo hayo jijini Dar es Salaam baada ya kumalizika kwa shughuli za kufanya usafi katika mitaa mbalimbali ya Kariakoo likiwemo kwanza eneo pia la Soko Kuu la Kariakoo.

Akieleza mbele ya wananchi na wafanyabiashara wa Kariakoo Mpogolo amesema katika kuhakikisha Kariakoo inakuwa safi ni wajibu wa kila mfanyabiashara kuwa sehemu ya kuunga mkono jitihada zinazoendelea ili mazingira kuwa safi wakati wote.

“Kwa wafanyabiashara hakikisheni mnakuwa na chombo cha kuhifadhia taka, na Maelezo haya sio ombi ni lazima, kila baada ya baada ya meza tatu kuwe na chombo cha taka.Kwa wafanyabiashara ambao katika meza zao kutakuwa na taka watatozwa faini na meza itaondolewa kwa wiki moja.

“Na kwa wakandari katika kila mtaa wa Kariakoo kuwe na chombo kikubwa cha kuhifadhi taka.Kukiwa na vyombo vikubwa kwa ajili ya kuhifadhia taka maana yake wafanyabishara vyombo vyao vinapokuwa vimejaa watapeleka katika vyombo vikubwa vilivyopo katika mitaa ya Kariakoo.”

Kuhusu mitaro ya maji kuziba katika mitaa mbalimbali ya Kariakoo,Mpogolo ametoa maelekezo kwa Wakala wa Barabara Tanzania(TANROAD) kuhakikisha wanaanza kazi ya kusafisha mitaro hiyo ili maji yatiririke.

Kwa upande wa taa za barabarani Mpogolo amesema Wilaya hiyo imejipanga vema na kusisitiza taa za barabarani zitawekwa katika maeneo yote yaliyokusudiwa huku pia akitoa rai kwa wamiliki wa majengo Kariakoo kuhakikisha nao wanafunga taa.

Pia ametoa onyo kwa wamiliki wa majengo yanayoendelea kujengwa Kariakoo kuacha tabia ya kuweka matofali,mchanga na kokoto kwa muda mrefu katika barabara za mtaani.

Kwa upande wake Diwani wa Kata ya Kariakoo jijini Dar es Salaam Haji Manara amesema siasa za Kariakoo ni usafi wa mazingira pamoja na utulivu kwa wafanyabiashara wakubwa na wadogo, hivyo usafi ndio kipaumbele kwao.

“Mkuu wa Wilaya ya Ilala jitihada zako kuhusu usafi tunaziona lakini pia tumekuwa na vikao vya mara kwa mara kuzungumzia na kuweka mikakati ya usafi.Pia tunajua dhamira ya Rais Samia Suluhu Hassan kuhusu Usafi kwa Jiji la Dar es Salaam.”

Manara amesema pamoja na usafi unaoendelea lakini bado kuna baadhi ya mitaa uchafu ni changamoto kutokana na mitaro mingi kuziba, pia kuna mitaa ambayo haipitiki kabisa hivyo ametoa ombi kwa Mkuu wa Wilaya ya Ilala kufungua mitaa hiyo,ombi ambalo limekubaliwa.



 

Benki ya NMB imeorodheshwa katika nafasi ya tisa duniani ndani ya Daraja la Sita la benki zenye mali ya kati ya Dola za Marekani bilioni 3 na bilioni 10. NMB ni miongoni mwa benki 500 kutoka nchi 89 zilizojumuishwa katika orodha ya Forbes ya World’s Top Performing Banks 2026.

Forbes na Statista zilifanya tathmini hiyo kwa kuzingatia uwezo wa kupata faida, ukuaji na ubora wa mapato, uimara wa mtaji na vyanzo vya fedha, pamoja na ubora wa mali na ufanisi wa uendeshaji. Mwaka 2025, NMB iliripoti faida baada ya kodi ya takribani Sh760 bilioni na mali ya Sh17.6 trilioni.

Mkurugenzi Mtendaji na Afisa Mtendaji Mkuu wa NMB Bank Plc, Ruth Zaipuna, amesema utambuzi huo unaakisi mageuzi ya muda mrefu ya benki na uwezo wa sekta ya benki Tanzania kushindana kimataifa.

Zaipuna amesema NMB itaendelea kutumia ukubwa wake, teknolojia, ushirikiano na uwezo wa kifedha kupanua upatikanaji wa mitaji katika kilimo, viwanda, biashara, miundombinu na uchumi wa kidijitali, ikiwa ni sehemu ya kusaidia utekelezaji wa Dira 2050.


Na. Jeshi la Polisi Dar es Salaam.

Katika kuhakikisha Jeshi la Polisi linaaendelea kujiimarisha katika Mafunzo na kutoa huduma Bora kwa Wananchi limeendelea kutoa mafunzo ndani na nje ya Tanzania kwa lengo la kuwajengea uwezo askari katika kutekeleza majukum kwa weledi na usasa ili kufanikisha adhima ya kutoa huduma bora kwa wananchi wanaolitegemea Jeshi hilo kwa ulinzi wao na mali.

Akiwaaga kwa niaba ya Mkuu wa Jeshi la Polisi Tanzania IGP Camillus Wambura Mkuu wa chuo cha Taaluma ya Polisi Dar es Salaam (DPA) Naibu Kamishna wa Polisi (DCP) Dkt Lazaro Mambosasa  amewataka Maafisa, Wakaguzi na Askari wa vyeo mbalimbali wanaokwenda kuhudhuria mafunzo nchini Indonesia, kutumia vyema fursa hiyo kwa kuzingatia masomo watakayopatiwa na kuhakikisha maarifa na ujuzi watakaoupata unakuwa chachu ya kuleta tija, ufanisi na usasa katika utendaji wa Jeshi la Polisi Tanzania, hususani katika utoaji wa huduma bora kwa wananchi.

Ameongeza kuwa Mkuu wa Jeshi la Polisi amesisitiza  washiriki hao wanatakiwa kuzingatia nidhamu, weledi na maadili ya Jeshi la Polisi wakati wote watakapokuwa nchini Indonesia huku akiwataka kuwakilisha vyema Tanzania na Jeshi la Polisi kwa kuhakikisha wanakuwa na mwenendo unaotoa taswira nzuri ya nchi yetu.

Aidha amewataka washiriki hao kutumia fursa hiyo kuitangaza Tanzania kwa kuonyesha sifa njema ya nchi yetu katika kudumisha amani, usalama na utulivu, pamoja na kutangaza vivutio vya utalii vilivyopo nchini ambapo pia amewataka kutangaza maeneo ya kipekee yenye umuhimu wa kihistoria na kiutalii, ikiwemo Bonde la Ngorongoro, ambalo ni miongoni mwa maeneo ya urithi wa dunia.

Dkt Mambosasa amebainisha kuwa Mafunzo hayo yanatarajiwa kujikita katika maeneo mbalimbali muhimu, yakiwemo, Uongozi na Maendeleo ya Kitaaluma (Professional Development and Leadership), Ushirikishwaji wa Jamii katika Ulinzi na Usalama (Community Policing) Teknolojia Zinazochipukia (Emerging Technologies), ikiwemo Akili Bandia (AI) Matukio Makubwa na Mbinu za Uchunguzi wa Jinai (High-Profile Incidents and Criminal Investigative Techniques) Mbinu Bora za Utendaji na Ubunifu (Best Practices and Innovations).

Sambamba na hayo ameweka wazi kuwa Masomo hayo yanatarajiwa kuwa chachu ya mabadiliko na maboresho katika utendaji wa kazi za kila siku wa Jeshi la Polisi Tanzania, kwa kuwawezesha washiriki kupata maarifa, ujuzi na uzoefu mpya utakaosaidia kuongeza ufanisi katika kutekeleza majukum ya Jeshi la Polisi.

Mafunzo hayo ya shirikisho la askari wa kike duniani na wasimamizi wa sheria IAWP yatahusisha nchi washiriki zaidi ya 64.





Na Farida Said Mkinga Tanga

Uwekezaji mkubwa unaotekelezwa na Chuo Kikuu Mzumbe kupitia ujenzi wa Kampasi ya Tanga, iliyopo Wilaya ya Mkinga mkoani Tanga, unatarajiwa kuwa chachu ya mageuzi ya kielimu, kijamii na kiuchumi katika eneo hilo.

Kampasi hiyo inatarajiwa kufungua fursa mbalimbali kwa wananchi wa Mkinga na maeneo jirani, ikiwemo upatikanaji wa elimu ya juu, huduma za afya, ajira, biashara pamoja na kuvutia uwekezaji katika maeneo mbalimbali.

Hayo yamebainishwa na Mkuu wa Chuo hicho ambaye pia ni Rais Mstaafu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Mwenyekiti Mstaafu wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Ali Mohamed Shein, alipofanya ziara katika eneo la ujenzi wa Kampasi hiyo lililopo Kata ya Gombero, Wilaya ya Mkinga.

Ziara hiyo imelenga kujionea maendeleo ya ujenzi wa Kampasi hiyo pamoja na kusisitiza umuhimu wa kukamilisha miundombinu iliyosalia ili Kampasi hiyo ianze kutoa huduma zilizokusudiwa.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Dkt. Shein amesema uwekezaji huo ni sehemu ya maono ya muda mrefu yenye manufaa mapana kwa jamii, akibainisha kuwa ubora wa majengo na miundombinu unaoonekana katika eneo hilo unaonesha dhamira ya Chuo Kikuu Mzumbe katika kujenga miundombinu endelevu itakayohudumia vizazi mbalimbali.

“Tunachokijenga hapa si kwa ajili yetu tu. Watakaokuja kunufaika zaidi ni watoto wetu, wajukuu zetu na vizazi vinavyofuata,” amesema Dkt. Shein.

Akitoa taarifa ya maendeleo ya ujenzi, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Mzumbe, Prof. William Mwegoha, amesema Kampasi hiyo ipo katika hatua za mwisho kuelekea kuanza kutoa huduma.

Amesema kazi kubwa iliyosalia ni ukamilishaji wa maeneo mbalimbali ya Kampasi, ambapo mkandarasi anaendelea na kazi hizo kabla ya miundombinu hiyo kuwa tayari kwa matumizi.

Kwa mujibu wa Prof. Mwegoha, kukamilika kwa ujenzi huo kutawezesha Kampasi kuanza kutekeleza majukumu yake na kutoa huduma mbalimbali zilizokusudiwa kwa jamii na wadau wengine.

Akizungumzia fursa zinazotokana na uwekezaji huo, Mwenyekiti wa Baraza la Chuo Kikuu Mzumbe, Balozi Modest Jonathan Mero, amesema uwepo wa Kampasi hiyo Mkinga ni fursa mpya ya maendeleo kwa jamii.

Amesema Kampasi hiyo itakuwa na mchango mkubwa katika sekta za elimu, afya, biashara na uwekezaji, huku mwingiliano kati ya wanafunzi, wataalamu na jamii ukiwa na nafasi muhimu katika kuchochea maendeleo ya eneo hilo.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Mkinga, Mhe. Gilbert Kalima, akimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Tanga, amesema Serikali itaendelea kushirikiana na Chuo Kikuu Mzumbe pamoja na wadau wengine kuhakikisha changamoto zinazoweza kuchelewesha matumizi ya Kampasi hiyo zinapatiwa ufumbuzi kwa wakati.

Aidha, Mhe. Kalima ametambua na kupongeza mchango wa viongozi wa vijiji waliowezesha upatikanaji wa eneo lenye ukubwa wa takribani ekari 300 kwa ajili ya ujenzi wa Kampasi hiyo.

Amesema upatikanaji wa eneo hilo umeweka msingi muhimu wa utekelezaji wa uwekezaji huo mkubwa, ambao unatarajiwa kuwa na manufaa ya muda mrefu kwa wananchi wa Mkinga na maeneo jirani.








Na mwandishi wetu

DODOMA. Kamishna wa Uhifadhi wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Profesa Dos Santos Silayo, amewataka watumishi wapya 328 kutumia mafunzo ya kijeshi na ukakamavu waliyopitia kujenga nidhamu, uadilifu na weledi katika kulinda rasilimali za misitu na nyuki nchini.

Profesa Silayo amesema hayo leo, Jumatatu, Septemba 14, 2026, wakati akifungua mafunzo elekezi kwa watumishi hao katika Chuo cha Mipango ya Maendeleo Vijijini (IRDP-Mipango), Dodoma.

Watumishi hao wamepitia mafunzo ya awali ya kijeshi na ukakamavu katika Kituo cha Mafunzo cha TFS, Mlele kwa miezi sita, kabla ya kuanza majukumu katika vituo mbalimbali nchini.

Akizungumza wakati wa ufunguzi huo, Profesa Silayo amesema mafunzo hayo hayakuwa mepesi, lakini yamewajengea nidhamu na ukakamavu unaohitajika katika kutekeleza majukumu yao kama askari wa uhifadhi.

Amewataka kufanya kazi kwa bidii, ubora na utu, huku wakiepuka rushwa, tamaa, uzembe na matumizi mabaya ya madaraka.

“Tufanye kazi hii kwa bidii, tuifanye kwa ubora wa hali ya juu, lakini tufanye kwa utu,” amesema.

Amesema watumishi hao wana taaluma mbalimbali, zikiwamo uhandisi, afya, manunuzi, uhasibu, misitu na nyuki, lakini wameunganishwa na dhamira moja ya kulinda na kuendeleza rasilimali za misitu na nyuki.

Pia amewataka kuheshimu viongozi na mfumo wa uongozi, kujifunza kutoka kwa watumishi waliowatangulia na kutumia taaluma zao kwa manufaa ya TFS na Taifa.

Baada ya kukamilisha mafunzo hayo elekezi, watumishi hao wanatarajiwa kupangiwa vituo mbalimbali vya kazi nchini.







Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Bara, Ndugu Stephen Wasira, amewasili leo mkoani Iringa, ambapo amepokelewa na viongozi wa Chama na Serikali wakiongozwa na Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Iringa, Komredi Daudi Yasin.

Ndugu Wasira amepokelewa katika Uwanja wa Ndege wa Nduli, mkoani Iringa, alipowasili kwa ajili ya shughuli mbalimbali za Chama.

Akiwa mkoani humo, pamoja na shughuli nyingine, Ndugu Wasira anatarajiwa kufungua Mafunzo ya Wakufunzi wa Chama yatakayofanyika katika Chuo cha Mafunzo cha Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM).






Wakulima katika Wilaya za Kondoa, Chemba na Bahi mkoani Dodoma wanatarajiwa kunufaika na taarifa sahihi za kiwango cha mvua zitakazonyesha kuanzia msimu ujao, kupitia vifaa vya kisayansi vilivyowekwa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) kwa kushirikiana na Shirika la  INADES-Formation Tanzania, hatua inayolenga kuwawezesha kufanya maamuzi sahihi ya kilimo, kuongeza uzalishaji na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Akizungumza Mkurugenzi Mtendaji wa INADES-Formation Tanzania, Bi. Jacqueline Nicodemus, amesema  changamoto kubwa iliyobainika katika utekelezaji wa mradi wa Mabadiliko ya Tabianchi katika sehemu kame unaotekelezwa na shirika hilo katika Wilaya za Bahi, Chemba na Kondoa, ni taarifa za utabiri wa hali ya hewa kutowafikia wakulima kwa namna inayowawezesha kuzitumia moja kwa moja katika mashamba yao.

Ameeleza kuwa taarifa nyingi huishia katika ngazi za wilaya na maeneo makubwa, wakati wakulima wanahitaji taarifa zinazohusiana na maeneo yao mahsusi, na kupitia ushirikiano na TMA, vifaa vya kisayansi vya kupima mvua vimewekwa katika vijiji mbalimbali, ikiwemo Kisima cha Ndege, Gwandi na Potea, ili kuwasaidia wakulima kupata taarifa sahihi za kiwango cha mvua na kuunganisha taarifa hizo na maarifa ya asili waliyonayo, ili kuwawezesha kufanya maamzi sahihi kwenye kilimo.

Kwa upande wake, Meneja wa TMA Kanda ya Kati Mussa Kidato,  amesema vifaa vya kupima mvua vilivyowekwa, vitawawezesha wakulima kupima kwa usahihi kiasi cha mvua inayonyesha badala ya kutegemea vipimo vya asili ambavyo havina uhakika wa kutoa takwimu sahihi, amesema taarifa hizo zitawasaidia wakulima kufanya maamuzi ya mazao gani walime, huku TMA ikiendelea kutoa elimu ya matumizi sahihi ya vifaa hivyo.

Akizungumzia manufaa ya hatua hiyo, Elizabeth Shoo, Afisa Maendeleo ya Jamii wa Wilaya ya Kondoa na Afisa Kiungo wa Mradi wa Mabadiliko ya Tabianchi unaotekelezwa na INADES-Formation Tanzania, amesema kipima mvua kitasaidia kufuatilia kiwango cha mvua kwa kupima na kurekodi taarifa kila siku, wiki na mwezi, ambapo taarifa hizo zitawawezesha wananchi kupanga shughuli za kilimo kwa uhakika zaidi, kuchukua tahadhari dhidi ya athari za mvua kubwa na kuongeza tija katika uzalishaji.

Kwa upande wake, Afisa Mradi kutoka INADES-Formation Tanzania, Paul Chugu, amewataka wananchi kutunza vifaa hivyo na kuhakikisha vinatumika kwa usahihi ili viweze kutoa matokeo yaliyokusudiwa, aidha amewataka wananchi waliopewa mafunzo ya kupima na kurekodi taarifa za mvua kuwa makini katika kutekeleza jukumu hilo, ili kuhakikisha takwimu zinazokusanywa ni sahihi na zinatumika ipasavyo katika kupanga shughuli za kilimo.

Akizungumza kwa niaba ya wananchi wa kijiji cha Potea Amina Juma Lungi, amesema kifaa hicho kitawasaidia wakulima kuachana na utegemezi wa vipimo vya asili na kupata taarifa sahihi za kiwango cha mvua, zitakazowawezesha kupanga shughuli zao za kilimo kwa ufanisi na kuongeza mavuno, ameahidi kuwa wananchi wa kijiji hicho watakitunza na kukitumia ipasavyo ili kiwe na manufaa kwa jamii.

Kwa ujumla, ushirikiano kati ya INADES-Formation Tanzania na TMA unalenga kuziba pengo la upatikanaji wa taarifa sahihi za mvua katika ngazi ya mkulima, kwa kuhakikisha takwimu zinazopatikana kupitia vipimo vya kisayansi zinawafikia wananchi kwa wakati na kwa namna inayoeleweka, Hatua hiyo inatarajiwa kuwawezesha wakulima kufanya maamuzi bora ya kilimo, kuongeza uzalishaji na kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi.









Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema kuundwa kwa Kamati ya Pamoja ya Majadiliano yenye wajumbe kutoka CCM na ACT Wazalendo ni hatua muhimu katika kuendeleza mchakato wa maridhiano na kuimarisha amani, umoja na utulivu wa kisiasa Zanzibar.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo tarehe 14 Septemba 2026, Ikulu Zanzibar, wakati wa uzinduzi rasmi wa Kamati hiyo, akiwataka wajumbe kutekeleza majukumu yao kwa uadilifu, kuheshimiana na kuweka mbele maslahi mapana ya Zanzibar na wananchi wake

Amesema Kamati hiyo ni mwendelezo wa utekelezaji wa makubaliano yaliyofikiwa baina ya CCM na ACT Wazalendo, huku akisisitiza umuhimu wa viongozi wa kisiasa na wadau wengine kuendelea kushirikiana katika kujenga Zanzibar yenye amani, utulivu na maendeleo.

Aidha, Rais Dkt. Mwinyi amewapongeza viongozi wa CCM, ACT Wazalendo, viongozi wengine wa kisiasa, wazee na Marais Wastaafu wa Zanzibar, Mhe. Dkt. Amani Abeid Karume na Mhe. Dkt. Ali Mohamed Shein, kwa mchango wao katika kuendeleza mchakato wa maridhiano.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa ACT Wazalendo, Mhe. Othman Masoud Othman, amesema chama hicho kiko tayari kuendelea kushirikiana katika kuijenga Zanzibar, akimpongeza Rais Dkt. Mwinyi kwa hatua mbalimbali alizochukua katika kusimamia mchakato wa maridhiano.

Katika hafla hiyo, Rais Dkt. Mwinyi amekabidhi Hadidu Rejea za Kamati kwa Wenyeviti Wenza, Ndg. Omar Ali Sheikh kutoka ACT Wazalendo na Ndg. Abdi Mahmoud Abdi kutoka CCM Zanzibar




















Top News