Na HABIBA MBARUKU, Mahakama-Dodoma
Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju amesema kuwa, Haki Jinai si mali ya Taasisi moja bali ni mfumo wenye Taasisi nyingi, wenye lengo la kuhakikisha haki inapatikana mapema ipasavyo kwa usawa, uadilifu na kwa kuzingatia Katiba na Sheria za nchi huku akieleza kuwa wadau wote wanapaswa kushirikiana kwa pamoja ili kuhakikisha haki haicheleweshwi bila sababu za msingi.
Mhe. Masaju ameyasema hayo wakati wa kufunga Mkutano wa Mahakama na Wadau wa Haki Kuhusu Ushirikiano na Mahusiano katika Utekelezaji Majukumu ya Utoaji Haki Mahakamani leo tarehe 17 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
“Haki jinai ni mfumo mmoja wenye taasisi nyingi lakini wenye lengo moja, yaani kuhakikisha kuwa haki inapatikana mapema ipasavyo tunapaswa kuzungumza kuhusu mfumo mzima kwa sababu udhaifu wa kiungo kimoja katika mnyororo wa haki jinai unaweza kuchelewesha haki kwa mfumo mzima,” amesema Jaji Mkuu.
Mhe. Masaju ametoa mfano wa Mtume Paulo anapozungumza kuhusu kanisa ambapo amesema, “ni kama mwili wa binadamu, kama ambavyo kuna mikono, macho, miguu, lakini hivyo vyote ndiyo vinakamilisha mwili. Yaani macho hayawezi kujifanya yenyewe ni bora kuliko mguu na vile viungo vilivyoonekana kama ni dhaifu, hivyo Mungu alivifanya kuwa vya maana zaidi lakini ukweli hapa wote hakuna kiungo dhaifu, hizi Taasisi zote ni muhimu.”
Ameongeza kuwa, jukumu la kwanza la sheria duniani kote ni kusimamia utawala wa sheria, amani na usalama katika jamii na jukumu la pili ni kukusanya kodi kwa ajili ya maendeleo mbalimbali na kuongeza kuwa hata Mwenyezi Mungu huko mbinguni aliweka sheria, na aliyekwenda kinyume na sheria aliwajibika kama ambavyo Lucifer alivyowajibika.
“Kwa hiyo, mkishakuwa zaidi ya mtu mmoja tu lazima mjiwekee sheria namna ya kufanya mambo yenu na kwetu Tanzania utawala wa sheria unapatikana katika Ibara ya 26 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na mfumo wowote lazima uwe unaongozwa na utawala wa sheria, hata Mwenyezi Mungu kule mbinguni aliweka sheria, na bwana mkubwa yule akiitwa Lucifer alipoasi akawajibika” amesema Mhe. Masaju.
Katika hatua nyingine Jaji Mkuu amefafanua kuwa, Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050 inasisitiza juu ya amani, usalama na utulivu, ulinzi wa haki, uhuru wa msingi, uimara wa Taasisi na utawala wa sheria ambao ni kipengele muhimu cha utawala bora kinachosaidia kujenga jamii yenye usawa, uwajibikaji, haki na kuaminiana.
Aidha, ameeleza kuwa, mashauri ya jinai hayaanzii mahakamani wala polisi pekee kwa kuwa vyombo hivyo vyote haviwi sehemu na wakati ambapo matukio hayo ya kihalifu yanatokea hivyo, wadau wote wanapaswa kuungana na kufanya kazi kwa pamoja kama ambavyo viungo katika mwili vinavyofanya kazi kwa pamoja na kutegemeana.
“Kesi ya jinai inaanza kwenye jamii huko tukio linapotokea, inaenda kwenye vyombo vya uchunguzi iwe ni Polisi, ni Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa, ni Mamlaka ya Kuzuia na Kupambana na Dawa za Kulevya, inaenda Ofisi ya Taifa ya Mashtaka, hatimaye kama kuna ushahidi inaenda mahakamani, na waliohusika kumkamata mshukiwa wanakuja kutoa ushahidi mahakamani kama amepatikana na hatia anarudi gerezani kwa ajili ya reform, utaona kwamba huu mnyororo ni mpana ni mnyororo mrefu lakini mnyororo imara, ” ameeleza Mhe. Masaju.
Katika hatua nyingine, amesema kuwa, ni vema kukawa na mtiririko mzuri wa kimfumo wa usimamizi wa mashauri ya jinai ili kuondoa changamoto zinazokwamisha mashauri kumalizika na kuongeza kuwa Mahakama haiwezi kuwa na ufanisi wa asilimia 100, ikiwa hatua zilizotangulia hazifanyi kazi mapema ipasavyo na kwa ufanisi na kwamba kunaweza kuwa na Mahakama yenye uwezo wa kusikiliza Mashauri Majaji na Mahakimu wenye uwezo lakini kama uchunguzi haujakamilika au kuwepo kwa changamoto yoyote shauri haliwezi kuendelea.
“Mahakama haiwezi kuwa na ufanisi wa asilimia 100 ikiwa hatua zilizotangulia Mahakama hazifanyi kazi mapema ipasavyo na kwa ufanisi. Tunaweza kuwa na Mahakama yenye uwezo wa kusikiliza mashauri, Majaji na Mahakimu wenye uwezo, na mifumo ya kielektroniki au miundombinu, lakini pia ni waadilifu. Lakini kama uchunguzi haujakamilika, jalada halijawasilishwa, mashahidi hawapatikani, maelezo hayajakamilika, hati za mashtaka zina kasoro, mshtakiwa hajaletwa mahakamani, au nyaraka muhimu hazijafikishwa mahakamani mapema, katika mtiririko kama huu kesi haiwezi kwenda mbele, hivyo ni vema kukawa na ile systematic flow ya criminal justice ya case management ili kuondoa hizo changamoto” amesisitiza Jaji Mkuu.
Akizungumza kuhusu uwajibikaji na kujituma, Mhe. Masaju amesema kuwa, kila Taasisi ya Haki Jinai inapaswa kuwajibika ipasavyo ili kuondoa ucheleweshaji wa mashauri bila kusubiri shauri lifike mahakamani huku akirejea Ibara ya 25 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo inasisitiza juu ya uwajibikaji na kujituma katika kila kazi kwa kufahamu chanzo cha kukwama kwa shauri, wapi lilipofikia katika utekelezaji, imefikia hatua zipi za ushahidi, jambo litakalosaidia mnyororo mzima wa haki jinai kufanya kazi vizuri.
Kadhalika, Mhe. Masaju amewakumbusha wadau wa Haki Jinai kwamba, mfumo unahitaji ushirikiano thabiti, mawasiliano ya karibu na uratibu mzuri ambayo ndio nguzo ya mafanikio hivyo, taasisi zote zifanye kazi bila kujitenga.
“Ni vyema tukumbuke kuwa, mfumo wetu wa haki jinai unahitaji ushirikiano thabiti (cooperation), mawasiliano ya karibu (communication), na uratibu mzuri (coordination). Hivi vitu vitatu yaani Cooperation, Communication, and Coordination ndivyo nguzo kuu za mafanikio yetu katika usimamizi wa haki jinai. Kama taasisi moja inafanya kazi kwa kujitenga au bila kutoa taarifa kwa nyingine, ni wazi kuwa, kutakuwa na kukwama kwa mashauri au kuchelewa kwa haki,” amesisitiza Jaji Mkuu.
Kadhalika, Mhe. Masaju amezitaka Taasisi za mnyororo wa Haki Jinai kuzingatia matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) na kuhakikisha mifumo inasomana ili kurahisisha mchakato mzima wa kuhakikisha haki inapatikana mapema ipasavyo bila kucheleweshwa na sababu zisizo na msingi.
Akihitimisha hotuba yake. Mhe. Masaju amezitaka Taasisi za mnyororo wa Haki Jinai kuchukua tahadhari juu ya uwepo wa mvua za El nino kwa kuhakikisha wanaweka miundombinu imara itakayowawezesha kufanya kazi pindi mvua hizo zitakapoanza kunyesha.
Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Majaji, Viongozi na Watumishi wa Mahakama pamoja na Wadau wa Haki Jinai wakati wa Mkutano wa Mahakama na Wadau wa Haki Kuhusu Ushirikiano na Mahusiano katika Utekelezaji Majukumu ya Utoaji Haki Mahakamani uliofanyika tarehe 17 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Aliyeketi kushoto ni Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Amir Mruma na kulia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga.
Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akitoa hotuba ya kufunga Mkutano wa Mahakama na Wadau wa Haki Kuhusu Ushirikiano na Mahusiano katika Utekelezaji Majukumu ya Utoaji Haki Mahakamani uliofanyika tarehe 17 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
Baadhi ya Viongozi, Watumishi wa Mahakama pamoja na Wadau wa Haki Jinai wakisikiliza hotuba ya Jaji Mkuu alipokuwa akifunga Mkutano wa Mahakama na Wadau wa Haki Kuhusu Ushirikiano na Mahusiano katika Utekelezaji Majukumu ya Utoaji Haki Mahakamani uliofanyika tarehe 17 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Amir Mruma akitoa neno wakati wa kufunga Mkutano wa Mahakama na Wadau wa Haki Kuhusu Ushirikiano na Mahusiano katika Utekelezaji Majukumu ya Utoaji Haki Mahakamani uliofanyika tarehe 17 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya akitoa taarifa ya utekelezaji wa mikakati kwa upande wa Mahakama wakati wa Mkutano kati ya Mahakama na Wadau wa Haki Kuhusu Ushirikiano na Mahusiano katika Utekelezaji Majukumu ya Utoaji Haki Mahakamani uliofanyika tarehe 17 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
(Picha na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)