Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.
Samia Suluhu Hassan anaondoka nchini leo kwenda Pretoria Africa ya
Kusini ambako atamwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.
John Pombe Magufuli katika Mkutano wa 37 wa Wakuu wa Nchi na Serikali
wa Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika utakaofanyika Pretoria,
Afrika Kusini tarehe 19 na 20 Agosti, 2017.
Mkutano
huo utapokea na kujadili ajenda mbalimbali ikiwemo uchaguzi wa
Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti wa SADC na Uchaguzi wa Mwenyekiti na
Makamu Mwenyekiti wa Asasi ya SADC ya Ushirikiano wa Siasa, Ulinzi na
Usalama; Hali ya Michango mbalimbali ya Nchi Wanachama na Kupokea
taarifa ya Mwenyekiti anayeondoka wa SADC Organ.
Pia
Mkutano utapokea taarifa ya Katibu Mtendaji wa SADC; Kupitia hali ya
kiuchumi katika Kanda ya SADC; Kuwasilisha Kaulimbiu ya Mkutano wa SADC;
Taarifa kuhusu Mfuko wa Maendeleo wa SADC; Taarifa ya Utekelezaji wa
Mpango Mkakati wa Viwanda; Kuwezesha Chuo cha Elimu ya Sayansi na
Teknolojia; Maombi ya Serikali ya Comoro na Serikali ya Burundi kujiunga
na SADC; Utekelezaji wa Mabadiliko ya Kitaasisi ya Umoja wa Afrika na
Mkutano wa Mshikamano kati ya SADC na Saharawi ya Magharibi.
Mkutano
huo utatanguliwa na Mkutano wa Dharura wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa
Troika Mbili ya SADC (SADC Double Troika Summit) tarehe 18 Agosti, 2017
ambao Tanzania itakabidhi nafasi ya uenyekiti kwa mwenyekiti mpya.
Double Troika inahusisha nchi wanachama sita ambao kwa sasa ni
Swaziland, Tanzania, Afrika Kusini, Angola, Botswana na Msumbiji. Katika
mkutano huo Mfalme Mswati III wa Swaziland atakuwa ndiye Mwenyekiti.
Ajenda kuu katika Mkutano huu ni kupokea na kujadili taarifa kuhusu hali
ya kisiasa, kiulinzi na kiusalama katika Kanda na hasa nchini DR Congo
na Lesotho.
Makamu wa
Rais amefuatana na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa
AfrikaMashariki, Mhe. Balozi Dkt Augustine Mahiga, Waziri wa Viwanda
Biashara na Uwekezaji, Mhe. Charles Mwijange, Naibu Waziri wa Fedha,
Mhe. Ashatu Kijaji na watendaji wengine waandamizi Serikalini
Makamu wa Rais na ujumbe wake anatarajia kurudi nchini Agosti 21, 2017.
Imetolewa na
Ofisi ya Makamu wa Rais
Dar es salaam
17/8/2017
Makamu wa Rais Mhe.Samia Suluhu Hassan akizungumza jambo na Mkuu wa Wilaya ya Temeke ,Felex Jackson katika Uwanja wa Ndege wa Julias Nyerere Dar es salaam leo Agosti ,17/2017 akielekea Nchini Pretoria Africa ya Kusini ambako atamwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. John Pombe Magufuli katika Mkutano wa 37 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika utakaofanyika Pretoria, Afrika Kusini tarehe 19 na 20 Agosti, 2017.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...