Na Evance Ng’ingo 

HIVI karibuni mfanyabiashara mkubwa nchini na Afrika nzima kwa ujumla, Mohamed Dewji, Moo alitekwa na watu wasiojulikana ambao hadi sasa jeshi la Polisi linaendelea kuwasaka. Habari za kutekwa kwa Moo zimetangazwa kwenye vyombo vya habari vya ndani na nje ya nchi ambapo kwa namna moja au nyingine limetia dosari taswira ya nchi hii inayosifika kwa amani duniani.

Tukio hilo limewashtua watu wengi ndani na nje ya nchi huku akiombewa apatikane akiwa salama, lakini pia kuna watu ambao wanatumia tukio hilo kama mwanya wa kuikosoa serikali kwa madai ya kuwa imeshindwa kumpata mfanyabiashara huyo hadi sasa. Wapo ambao wanalibeza jeshi la Polisi kuwa limeshindwa kumsaka na kumpata mfanyabiashara huyo huku wengine wakidai kuwa limeshindwa kukabiliana na matukio ya utekwaji watu nchini.

Kwa mujibu wa takwimu zilizotolewa na Jeshi hilo hivi karibuni linaonesha kuwa mwaka juzi, walitekwa watu tisa ambapo watano walipatikana wakiwa hai na wanne hawajulikani walipo hadi sasa huku watuhumiwa sita wamekamatwa na kufikishwa mahakamani na mmoja aliuliwa na wananchi.

Mwaka 2017 walitekwa watu 27 ambapo 22 walipatikana wakiwa hai, wawili wamekufa huku watatu hadi sasa hawajapatikana watatu wamefariki huku watu 11 wamefikishwa mahakamani. Kwa mwaka huu Januari hadi Oktoba watu 21 walitekwa na Jeshi limewaokoa 17 huku wanne hawajapatikana hadi sasa na watuhumiwa 10 wamefikishwa mahakamani.
Kwa takwimu hizi zinaashilia kuwa jeshi hilo linaweza kukabiliana na matukio ya utekwaji nchini licha ya changamoto za kiteknolojia zinazolikabili. Binafsi ningependa kuwasihi wanasiasa na watu wengine mbalimbali kuwa na imani na jeshi hilo katika kumsaka na kumpata mfanyabiashara huyo tajiri.

Tukio la kutekwa kwa mfanyabiashara mkubwa wa kiwango cha Mo ni la kwanza kutokea nchini hasa ikizingatiwa kuwa takwimu za waliotekwa hakuna mfanyabiashara wa kiwango cha Mo hivyo ni tukio linalohitaji umakini zaidi. Utekwaji wa aina hii unahitaji nguvu ya ziada katika kuukabili na kuwa jeshi la Polisi peke yake haliwezi kufanikisha bila ya kuwapo kwa ushirikiano thabiti wa wananchi.

Ushirikiano huo wa wananchi sio tu kuishia kusaidia kupatikana kwa Mo lakini pia ni pamoja na kushiriki katika kuwafichua watu wenye tabia za utekaji kwa ujumla. Jamii ikishiriki kikamilifu ni wazi kuwa matukio kadhaa ya utekwaji hayataendelea kuwapo nchini hasa ikizingatiwa kuwa tangia mwaka juzi kumekuwa na matukio ya aina hiyo.

Lakini pia ni lazima kwa hoteli na maeneo makubwa ambayo hutembelewa na watalii nchini kuhakikisha kuwa yanalindwa na walinzi kutokea kwenye kampuni zenye uzoefu na uwezo mkubwa wa ulinzi.

Pia ufungwaji wa kamera za kurekodia matukio ni muhimu zaidi katika kuwafichua kwa urahisi watekaji na wahalifu wengine kwa ujumla. Watanzania, wanasiasa, viongozi wa dini, wasomi na jamii nzima kwa ujumla tushirikiane kukemea matukio ya utekwaji wa watu ili kunusuru haiba ya nchi yetu.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...