Na Said Mwishehe,Globu jamii
KAIMU Balozi wa Marekani hapa nchini Dk. Imni Patterson, ameishauri Tanzania njia muhimu za kifikia uchumi wa kati na wa viwanda.

Ushauri huo ameutoa leo jijini Dar es Salaam, alipokuwa akizungumza na Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania Geoffrey Mwambe wakati wa mazungumzo yao ambayo yalihusu kujadili namna ya kuboresha mazingira ya uwekezaji nchini.

Pia Kaimu Balozi huyo ameihakikishia Serikali ya Tanzania kwamba itatoa kila aina ya ushirikiano ili kufanikisha Tanzania ya viwanda.

"Ubalozi wa Marekani,nchi ya Marekani na Wamarekani wote waliopo nchini Tanzania wapo tayari kusaidiana na serikali katika kuhakikisha nchi ya viwanda inafanikiwa," amesema.

Dk.Imni ameshauri 
kwa Serikali ya Tanzania kuwa ili ifanikiwe kwenye uchumi wa viwanda ni vema ikaendelea kushirikiana na sekta binafsi katika kufanikisha uwekezaji na amefurahishwa na mazungumzo ambayo ya Serikali ya Tanzania inayoyafanya kati yake na sekta binafsi.

"Hakuna nchi ambayo inaweza kufikia nchi ya viwanda bila kushirikisha sekta binafsi pamoja na wawekezaji wa ndani na nje.Hivyo ni vema sekta binafsi zikapewa fursa katika uwekezaji ili kufikia Serikali ya Viwanda ambayo sisi tunaiunga mkono," amesema.

Kuhusu mazungumzo yao amesema yamejikita katika kukuza biashara ,uwekezaji na kukuza uchumi na kwamba kutokana na mazingira mazuri yaliyopo ni imani yao Tanzania itafikia malengo ya kuwa nchi ya viwanda.

Kwa upande wake Mwambe amesema TIC jukumu lao ni kukutanisha sekta mbalimbali za Serikali na binafsi ambapo mabalozi wa Tanzania waliopo nchi mbalimbali wanahakikisha wanashiriki kikamilifu kuvutia wawekezaji.

Amefafanua hivyo ubalozi wa Marekani nchini kupitia Kaimu Balozi wake wamekuwa na wajibu wa kuhamasisha uwekezaji baina ya nchi hizo mbili.

"Ni jukumu lake kuhamasisha wawekezaji wa Marekani kuja Tanzania kuwekeza.Tunafahamu juhudi za Serikali ya Marekani katika kuisaidia Tanzania kwa kuhakikisha inajiimarisha kiuchumi," amesema.

Amesema jitihada za Kaimu Balozi zimesaidia kufanikisha kwa ujio wa kundi la wafanyabiashara wa Florida kuja nchini kwa ajili ya kuangalia mazingira ya uwekezaji na kwamba watakuja siku za karibuni.

" Tumezungumzia maeneo mbalimbali ambayo tunaweza kushirikiana ili kutimiza malengo ya Serikali ya kutekeleza uwekezaji nchini. Kama nchi tunataka kuendelea,lazima tutafute njia sahihi za kuendeleza mifumo ya uwekezaji.

"Tunataka kujenga nchi,hivyo tuna jukumu kubwa la kujenga sekta binafsi na tukiwa na private sekta tutakwenda vizuri kama Taifa.Sisi TIC tutahakikisha sekta binafsi inaimarika na maamuzi ya Serikali ni kuijenga sekta binafsi na mjumbe wa bodi yangu ni mtu mmoja kutoka Taasisi ya Sekta Binafsi Bw.Godfrey Simbeye," amefafanua.

Ameongeza Serikali yenye rushwa huwa haikusanyi kodi na huo ni msemo maarufu wa Mwalimu Nyerere, hivyo jukumu lililopo ni kuhakikisha rasilimali zilizopo zinatunufaisha wote."TIC tunataka kutengeneza umoja na mazingira yanayokubalika kwenye uwekezaji zaidi". 
Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania(TIC) Geoffrey Mwambi(kulia) akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam baada ya kufanya mazungumzoa Kaimu Balozi wa Marekani hapa nchini Dk.Imni Patterson.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...