Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mheshimiwa Dkt. Damas Ndumbaro (Mb) anaongoza ujumbe wa Tanzania katika Mkutano wa 18 wa Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya nchi za mwambao wa Bahari ya Hindi unaofanyika Durban, Afrika Kusini leo tarehe 2 Novemba, 2018. 

Mkutano huu umetanguliwa na Kikao cha 20 cha Makatibu Wakuu na Maafisa Waandamizi tarehe 31 Oktoba hadi tarehe 01 Novemba, 2018 ambapo ujumbe huo uliongozwa na Balozi Ramadhan M. Mwinyi, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.

Jumuiya ya nchi za mwambao wa Bahari ya Hindi (Indian Ocean Rim Association – IORA) ilianzishwa mwaka 1997 awali, ikijulikana kama Indian Ocean Rim Association for Regional Cooperation IORA-AC kabla ya kubadilishwa kuwa IORA mwaka 2013. Jumuiya hii inaundwa na nchi wanachama 21 ambazo ni Afrika Kusini, Australia, Bangladesh, Comoro, India, Indonesia, Jamhuri ya Kiislam ya Iran, Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kenya, Malaysia, Madagascar, Mauritius, Msumbiji, Shelisheli, Singapore, Somalia, Sri Lanka, Sultani ya Oman, Thailand, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) na Yemen. Tanzania ni moja kati ya nchi waanzilishi wa Jumuiya hii.

Katika muundo wake, IORA pia ina washirika wa mazungumzo (Dialogue Partners) saba (7) ambao ni Jamhuri ya Watu wa China, Japan, Marekani, Misri, Uingereza, Ufaransa na Ujerumani ambao hushiriki katika utekelezaji wa mipango mbalimbali ya Jumuiya.

Katika uongozi, Afrika Kusini ndie Mwenyekiti wa sasa wa IORA akisaidiana na Umoja wa Falme za Kiarabu kama Makamu Mwenyekiti. Hivyo, Mheshimiwa Lindiwe Sisulu (Mb), Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Kusini aliongoza mkutano huu.
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro akiwa kwenye Mkutano wa 18 wa Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya nchi za mwambao wa Bahari ya Hindi (IORA) unaofanyika Durban, Afrika Kusini kuanzia tarehe 2 Novemba, 2018. Mhe. Dkt. Ndumbaro anaongoza ujumbe wa Tanzania katika Mkutano huo ambao pamoja na mambo mengine nchi hizo zimekubaliana kuendelea kushirikiana katika kutekeleza miradi ya maendeleo iliyo chini ya maeneo tisa vipaumbele kwa IORA ambayo ni usalama na ulinzi wa bahari; biashara na uwekezaji; usafiri wa bahari; uvuvi; menejimenti ya udhibiti wa majanga; taaluma, sayansi na teknolojia; utalii na utamaduni; uchumi bahari; na uwezeshaji wanawake. Mwingine katika picha ni Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Ramadhan M. Mwinyi
Mkutano ukiendelea
Picha ya pamoja ya Mawaziri

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...