Na. Josephine Majura na Peter Haule WFM, Dodoma
Serikali imezitaka taasisi zote ambazo bado hazijajiunga na Mfumo wa Kielektroniki wa Ukusanyaji wa Mapato ya Serikali (GePG) kuhakikisha wamejiunga na mfumo huo kabla ya Juni 30, 2019.
Agizo hilo limetolewa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango Dkt. Khatib Kazungu, kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Bw. Doto James, wakati wa Mkutano wa mwaka wa wadau wa utumiaji wa mfumo wa GePG Jijini Dodoma.
Dkt. Kazungu, alisema kuwa hakutokuwa na fedha yoyote ya umma itakayokusanywa nje ya Mfumo wa GePG, hivyo wakati mwafaka wa kujiunga na kuunganishwa na mfumo huo ni sasa. “Napenda kusisitiza kuwa, ni lazima kutumia mfumo huu kwa kuwa unaongeza ufanisi na uwazi katika ukusanyaji wa Fedha za Umma na pia utaratibu wa matumizi ya GePG unatoa fursa ya kuwa na njia nyingi za kulipia na kuwapa walipaji wa huduma za Serikali utaratibu rafiki wa kufanya malipo”, alieleza Dkt. Kazungu.
Utaratibu wa makusanyo kabla ya mfumo wa GePG haukua rafiki kwa kuwa ilikuwa ni vigumu kuthibitisha malipo na pia kuwa na foleni ndefu kwenye Ofisi za Serikali zilizosababishwa na zoezi la kufanyiwa tathmini ya malipo ya huduma na kuthibitisha malipo. Alisema ili kukabiliana na changamoto hizo katika ukusanyaji wa Fedha za Umma, Juni 2017, Serikali iliifanyia marekebisho Sheria ya Fedha za Umma (PFA) ya mwaka 2001 na kuongeza kipengele kinachotaka Fedha zote za umma zikusanywe kupitia Mfumo wa Government e-Payment Gateway (GePG).
Mkurugenzi wa Mifumo ya Fedha wa Wizara ya Fedha na Mipango Bw. John Sausi, akieleza kuhusu bidhaa mpya zitakazo wasilishwa kwa wadau wa mfumo wa ukusanyaji mapato (GePG) wakati wa Mkutano wa wadau hao uliofanyika katika ukumbi wa Kambarage Jijini Dodoma.
Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango Dkt. Khatibu Kazungu ambaye ni mgeni rasmi akifungua mkutano wa wadau wa mfumo wa ukusanyaji mapato (GePG) wa uliofanyika katika ukumbi wa wa Wizara ya Fedha na Mipango (Kambarage) Jijini Dodoma.
Baadhi ya Washiriki wa mkutano wa mwaka wa mfumo wa ukusanyaji mapato (GePG), wakifuatilia hotuba ya mgeni rasmi Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango Dkt. Khatibu Kazungu (hayupo pichani), uliofanyika katika ukumbi wa Kambarage Jijini Dodoma.
Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango Dkt. Khatibu Kazungu ambaye ni mgeni rasmi akiwa katika picha ya pamoja na washiriki wa Mkutano wa mwaka wa watumiaji wa mfumo wa ukusanyaji mapato uliofanyika katika ukumbi wa Wizara ya Fedha na Mipango, Kambarage Jijini Dodoma. (Picha na Josephine Majura MoFP Dodoma)
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...