Na Said Mwishehe,Globu ya jamii

KAMA binadamu wa kawaida ninayeishi kwenye dunia hii ambayo muumba wa mbingu na ardhi ameitengeneza kwa umaridadi mkubwa huwa inafika mahali nakumbuka zamani.

Zamani yangu mimi Said Mwishehe.Zamani ambayo ni tofauti na zama hii ya sasa.Huwa namshukuru Molla kwa kunipa nafasi ya kuishi ile zamani yangu na sasa.Hakika huwa naangalia watoto na vijana wa sasa na aina ya maisha yao na kisha narudisha kumbukumbu zamani yangu.Zamani ambayo mawasiliano yetu yalitawaliwa na barua ambazo ili ifike kwa mhusika unampa dereva au kondakta wa basi ili ifike unakota iende.

Naizungumzia zamani ambayo barua unaweza kuituma kwa njia ya posta na kisha inamfikia muhisika bila tatizo.Zamani ambayo nilikuwa nasubiri niitwe mbele ya wanafunzi wengine shuleni kwa ajili ya kupewa barua.Siku ambayo nitapewa barua mbele ya wanafunzi najiona bonge la mtu.Yaani mtu ni mimi tu na wengine ni viumbe tu wa duniani.

Naikumbuka zamani ambayo hakukuwa na filamu za akina Sulatani chini ya uhusika wa Mtukufu Suleiman.Zamani ambayo naiuzungumzia ni ile iliyotaliwa na michezo ya kombolela.Zamani ambayo watoto walifurahia maisha yao halisi ya Mtanzania.Naizungumzia zamani ambayo watoto walijifunza maisha ya familia kupitia michezo ya baba na mama .Ukweli naikumbuka zamani ambayo watoto walifundishwa namna ya kuishi maisha mema.Zamani ambayo mtoto alikuwa wa jamii na akikosea anapewa adhabu na mzazi yoyote.

Naizungumzia zamani ambayo watoto tulishindana kutengeneza watoto wa udongo.Zamani ambayo tulishindana kutengeneza magari kwa kutumia maboksi, mabati au waya za umeme.Zamani ambayo hatukuwa na ujeri kwani tulikuwa tunatumwa na mtu yoyote ambaye amekuzidi umri.

Sizungumziii maisha ya watoto wa sasa ambao wengi wao wamekosa malezi halisi ya baba na mama.Watoto ambao wanalelewa na 'House Girl' na 'House Boy' .Siizungumzii sasa ambayo watoto wanapelekwa kuoga kwenye bwawa la kuogelea a.k.a Swimming Pool.Jamani naikumbuka zamani ambayo watoto tulienda kuoga mtoni.Zamani ambayo tunashinda kucheza kidali poo ndani ya maji.

Naizungumzia zamani ambayo shuleni tulikwenda kwa miguu .Zamani ambayo hakuna aliyefikiria kupanda School Bus.Zamani ambayo watoto walivalisha viatu vya DH. Naikumbuka zamani ya viatu vya Laizoni.Zamani ambayo watoto walivaa nguo za ndani za kiume za VIP.Usiombee ikatike kwani ilikuwa inapanda hadi kifuani.

Naizungumzia zamani ambayo siku nyumbani kukipwa wali ...unaoga saa 12 jioni kusubiri ubwabwa.Naikumbuka zamani ambayo haikuwa na papara ya maisha.Kimepatikana sawa kikikosena Ishallah.Naizungumzia zamani ambayo mtoto alikuwa wa mwisho kunawa wakati wa chakula.Zamani
ambayo mtoto alilazimika kupewa nyama ndio ale.Kinyume na hapo ataishia kuziona kwenye bakuli.

Naikumbuka zamani ambayo chakula kiliwekwa kwenye sahani moja na watoto wakala kwa pamoja.Zamani ambayo baba aliweza kujua tabia ya mtoto.Zamani ambayo mama alijua tabia ya mtoto wa kike.Zamani ambayo mtoto wa miaka mitano au sita aliweza kufua nguo zake.Siizungumzii sasa ambayo mtoto wa miaka 13 nguo zake anafuliwa na house girl.

Sasa ambayo mtoto anawekewa chakula kwenye sahani yake.Sasa ambayo mtoto ndio mwenye kutoa maagizo kwa mzazi anataka kula nini, anataka kuvaaa nini.Sitaki kabisa kuizungumzia sasa.Naikumbuka zamani, zamani ambayo kwenye harusi hakukua na kadi za kuingilia getini.Zamani ambayo watu walikaribishana chakula .Zamani ambayo kila mtu alikuwa ndugu wa mwingine.

Mimi Said Mwishehe yaani mimi Said naikumbuka zamani ambayo maisha ya nyumbani yalikuwa yanafuraha na watoto wote ni sawa.Zamani ambayo watoto wote tuliishi maisha ya kufafana.Maisha ambayo nguo mpya zitapatikana wakati wa sikukuu.Zamani ambayo haikuwa na utitiri wa wasanii
wa muziki wa kizazi kipya.

Zamani ambayo haikuwa na Bongo Muvi.Naizungumzia zamani ya akina Yondo Sister.Zamani ya akina Rambo na Bluce Lee.Zamani ambayo Pepe Kale alisikika bila tatizo.Zamani ambayo nyimbo za akina Mbaraka Mwinshehe zilipewa nafasi ya kusikika na redio Tanzania.Naikumbuka zamani ambayo ili uende kuanza darasa la kwanza lazima mkono uzunguke kichwa kwa juu na kushika sikio.

Hivyo wazazi walikuwa na kazi ya kutufanyisha mazoezi ya kushika sikio.Zamai ambayo mtoto alianza darasa la kwanza hata akiwa na umri wa miaka 10,11 au miaka 12 poa tu.Kwani kitu gani bwana wakati kikubwa ni elimu.

Sitaki kuizungumzia sasa kwani ni sasa ambayo ina kera.Sasa ambayo mwanaume anapiga goti anapomvisha pete ya uchumba binti wa kike.Sasa ambayo mwanaume anamwaga chozi hadharani kisa amependa.Naikumbuka zamani ambayo mtoto wa kike alipiga goti kwa mumewe.Alilia kuonesha hisia
za upendo kwa mwenza wake.

Yaani naomba nieleweke tu sitaki kuizungumzia sasa ambayo wazazi walio wengi hawana habari na watoto wao.Sasa ambayo mtoto wa kike anamiliki simu ya shilingi milioni moja na mzazi wala hana nafasi ya kuuliza imetoka wapi.Sasa ambayo mtoto wa kiume anashinda kwenye vijiwe vya kuvuta bangi na dwa za kulevya.

Sasa ambayo baba na mtoto wanashindana kwenye kubeti na mkeka ukichanika wote wanabaki wakiwaza.Eti kamkosa muhindi.Ujue sitaki kuizngumzia sasa ambayo utu umetoweka duniani.Sasa ambayo ndugu wanakutana siku ya msiba tu.Sasa ambayo hakuna mwenye habari na mwingine.Wenyewe wanasema kila mtu na maisha yake.Naikumbuka zamani ambayo ili uende kucheza baba au mama anakwambia imba tebo ya kwanza hadi ya 12.Zamani ambayo bibi na babu walitufundisha hadithi za kale.Hadithi ambazo zilitufundisha mambo mengi ya kwenye maisha.Naikumbuka zamani ambayo ukiwa darasa la tatu unafundishwa kupiga pasi nguo, unafundishwa namna ya kufagia.Unafundishwa kuheshimu
jamii inayokuzunguka.

Zamani ambayo haikuwa na wimbi la matapeli.Zamani ambayo watu walikuwa wakweli .Zamani ambayo tulishindana kuonesha vipaji vyetu shuleni.Zamani ambayo walipatikana mabingwa wa hesabu baada ya shule kushindana kwa ngazi ya mbalimbali hadi ya kitaifa.Zamani ambayo watoto walionesha umahiri wao katika fani mbalimbali.Sitaki kuizungumzia sasa ambayo watu wanashindana kwenye mitandao ya kijamii kwa ajili ya kuonesha mambo ya hovyo.Unabisha nini?Kumbuka ya Amber Ruty na mpenzi wake.Acha niikumbuke zamani.Sitaki kuingia kwenye malumbano,kisa nazungumzia ya sasa.
Inatosha bwana...yaani imetokea tu nimeikumbuka zamani.Sijui nini

kimetokea ila ndio hivyo tena zamani itabaki kuwa zamani.Zamani ambayo barua ilianza kwa kusema "Wewe uliye mbali na upeo wa macho yangu.Mimi ni mzima wa afya , hofu ni kwako.Upatapo barua hii utambue ndugu yako nimekukumbuka na nakupenda sana.Baba na mama wanakusalimia."Naikumbuka zamani ambayo hata hii namba ya simu 0713833822 sikuwa nayo.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...