Na Said Mwishehe,Globu ya jamii
HATIMAYE Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali(CAG) mstaafu Ludovick Utouh amevunja ukimya baada ya kueleza kuwa CAG ndio jicho la wananchi katika kuangalia mali za umma, hivyo haoni sababu ya kuibuka kwa mjadala bungeni kuhusu CAG.
Utouh amesema hayo leo Aprili 12,2019 jijini Dar es Salaam baada ya kufungua Mkutano wa Pili wa Taasisi ya Wanawake Wahasibu Tanzania(TAWCA) ambapo waandishi wa habari walitaka kupata kauli yake kuhusu kinachoendelea kati ya Bunge na CAG Proesa Mussa Assad.
"Mali za umma ni mali za wananchi, hivyo CAG ndio jicho lao katika kuhakikisha mali zao ziko salama na aachwe afanye kazi yake ,na ripoti kwenda bungeni maana yake ni kwamba kule ndiko waliko wawakilishi wa wananchi.Sioni sababu ya kuwepo kwa mjadala wa kibunge dhidi ya CAG ambao hauna tija yoyote,"amesema Utouh.
Hata hivyo, amesema ipo haja kwa Wahasibu wengi wakiwamo Wanawake Wahasibu kuhakikisha wanashiriki katika kuwania nafasi za uongozi ikiwemo bungeni ili wakiwa huko watasaidia kuweka mambo sawa ."Kama kutakuwa na wahasibu wengi bungeni maana haya mambo yanayoendelea sasa hayawezi kuwepo kwasababu watakuwa wanajua kuhusu ripoti ya CAG,amesema Utouh wakati anazungumza na Wanawake Wahasibu nchini.
Kwa kukumbusha tu Profesa Assad ameingia kweye mgogoro kati yake na Bunge baada ya kudai Bunge ni dhaifu kwa kushindwa kutekeleza mapendekezo ya Ripoti ya CAG.Baada ya kutolewa kwa kauli hiyo Bunge kupitia kwa Spika Job Ndugai liliamua kumjia juu kwa kumtaka kuomba radhi.
Siku za hivi karibuni Bunge lilitoa azimio la kutofanya kazi na Profesa Assad kwa madai ameshindwa kuomba radhi huku Spika Ndugai akisema kuwa watafanya kazi na ofisi ya CAG na sio Profesa.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...