Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na
Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula akipata maelezo kuhusiana na
Mradi wa Nyumba za Shirika la Nyumba za Taifa (NHC) uliopo eneo la
Ilembo Manispaa ya Mpanda mkoa wa Katavi kutoka kwa Meneja Mawasiliano
wa Shirika hilo Muungano Saguya jana wakati akikagua utekelezaji wa
miradi ya NHC mkoani Katavi. Wa kwanza kulia ni Mkuu wa wilaya ya Mpanda
Lilian Matinga na kushoto ni Kaimu Meneja wa NHC mkoa wa Katavi na
Rukwa Msumbuko Majaliwa.
Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na
Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula akioneshwa eneo inapojengwa
ofisi ya Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) katika halmashauri ya
wilaya ya Mlele mkoa wa Katavi na Meneja wa TFS Mlele Godfrey Mlele
(Kulia) wakati wa ziara yake ya kukagua miradi inayotekelezwa na Shirika
la Nyumba la Taifa (NHC) katika mkoa wa Katavi jana. Wa pili kushoto
ni Mkuu wa wilaya ya Mlele Recho Kasanda na wa pili kulia ni Meneja
Mawasiliano wa NHC Muungano Saguya
Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na
Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula na Mkuu wa wilaya ya Mpanda
Lilian Matinga wakiangalia jengo la Biashara la Paradise lilipo
halmashauri ya Manispaa ya Mpanda jana wakati wa ziara yake ya kukagua
utekelezaji wa miradi ya Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) katika mkoa
wa Katavi.
(PICHA ZOTE NA WIZARA YA ARDHI).
*********************************
Na Munir Shemweta, WANMM KATAVI
Naibu Waziri wa
Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula amelipongeza
Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) mkoa wa Katavi kwa kuwa moja ya mkoa
wenye miradi mingi ya Shirika hilo.
Dkt Mabula alitoa
pongezi hizo jana wakati akikagua miradi ya NHC kwenye mkoa wa Katavi
akiwa katika ziara yake ya kukagua utendaji kazi wa sekta ya ardhi
pamoja na ujenzi wa miradi inayotekelezwa na Shirika la Nyumba la
Taifa.
Miradi
aliyoikagua Naibu Waziri Mabula katika mkoa wa Katavi ni ujenzi wa
nyumba za watumishi katika Halmashauri ya wilaya ya Mlele, Ofisi na
Nyumba ya Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) pamoja na ukumbi wa
halmashauri ya Manispaa ya Mpanda. Pia alikagua mradi wa nyumba sabini
za Ilembo ambapo Nyumba kumi kati ya hizo ziliuzwa na nyumba sitini
zimepangishwa.
Alisema, mkoa wa
Katavi unaweza kuwa mkoa wa kwanza ama wa pili kwa kuwa na miradi mingi
ya Shirika la Nyumba la Taifa na hali hiyo siyo tu inaonesha jinsi
Shirika lilivyo makini kwenye uwekezaji miradi mbalimbali kama vile
ujenzi wa nyumba za kuuza, kupangisha na majengo ya biashara bali
inalifanya kuimarika kimkoa.
Akigeukia mradi
wa Jengo la Biashara la Paradise lililopo Manispaa ya Mpanda, Dkt Mabula
alilisifu jengo hilo kwa kuwa na mazingira mazuri ya kibiashara na
kushauri taasisi za serikali katika mkoa wa Katavi kutumia fursa ya
kupanga na kuwekeza kwenye jengo hilo kwa kuwa gharama zake ni nafuu
ukilinganisha wapangishaji wengine.
Aidha, amelitaka
Shirika la NHC mkoa wa Katavi kuhakikisha inalifanyia matangazo jengo
hilo la biashara la Paradise kwa lengo la kuvutia wateja kupanga hasa
ikizingatiwa kutolitangaza kunaweza kusababisha kukosa wateja.
Kauli hiyo ya
kutaka kufanyika matangazo kwenye jengo hilo inafuatia Naibu Waziri
Mabula kuelezwa na Kaimu Meneja wa Shirika la NHC mkoa wa Katavi na
Rukwa Masumbuko Majaliwa kuwa mpaka sasa jengo hilo la kibiashara
limepangisha asilimia thelathini tu ya wateja.
‘’Mrudi kwenye
kutangaza miradi yenu kupitia kipindi cha Maisha ni Nyumba na
ikiwezekana kazi hiyo ifanyike mkoa kwa mkoa na mhakikishe miradi yenu
mnaifanya kwa kasi, viwango na wakati ili kujenga trust kwa wateja’’
Alisema Dkt Mabula.
Kwa upande wake
Meneja Mawasiliano wa NHC Muungano Saguya alisema, kwa sasa Shirika lake
linafanya vizuri katika masuala ya ujenzi jambo lililosababisha
kuaminwa na serikali ambapo katika mji wa serikali eneo la Mtumba Dodoma
liliweza kujenga majengo ya Wizara nne na sasa Shirika linaendelea na
utekelezaji wa miradi mingine kama vile ujenzi wa nyumba na ofisi za
Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) nchi nzima.
Awali Kaimu
Meneja wa Shirika la Nyumba mkoa wa Katavi na Rukwa Masumbuko Majaliwa
alimueleza Naibu Waziri kuwa kwa sasa NHC mkoa wa Katavi inatekeleza
miradi mbalimbali katika mikoa ya Katavi na Rukwa.
Alisema katika
mkoa wa Katavi Shirika la Nyumba linatekeleza miradi ya nyumba za
watumishi Mlele, ukumbi wa manispaa ya Mpanda pamoja na ujenzi wa nyumba
za walimu Kibaoni wakati upande wa mkoa wa Rukwa miradi inayotekelezwa
ni ile ya mradi wa nyumba za makazi jangwani Sumbawanga pamoja na duka
la dawa katika hopspitali ya rufaa mkoa wa Rukwa.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...