Kaimu Mkuu wa Kanda ya Kati wa Shirika la Viwango Tanzania, Bi. Salome Emmanuel,
akiwaonesha waandishi wa habari bidhaa zisizokidhi viwango na kuisha muda wake
wa matumizi wakati wa zoezi la
uteketezaji wa bidhaa hizo lililofanyika leo Januari 16, 2020 katika dampo la
Chidaya Jijini Dodoma.
Sehemu
ya bidhaa zilizokamatwa kwenye zoezi la kubaini bidhaa zilizoisha muda wa matumizi zikiwa
tayari kuteketezwa leo Januari 16, 2020 katika Dampo la Chidaya Jijini Dodoma.
Oparesheni hiyo imefanikiwa kukamata bidhaa zenye thamani ya shilingi milioni kumi.
Mtambo
maalum unaotumika kuteketeza taka na bidhaa katika dampo la Chidaya Jijini
Dodoma ukiendelea na kazi ya kuteketeza bidhaa zilizoisha muda wa matumizi
zilizokamatwa kwenye zoezi lililoendeshwa na Shirika la Viwango Tanzania kwenye
mikoa ya Dodoma na Singida kati ya mwezi Oktoba na Desemba 2019.(Picha
zote na MAELEZO).
Na Mwandishi wetu
Shirika la Viwango Tanzania (TBS) limeteketeza bidhaa zenye thamani ya shilingi milioni 10 kwa kukosa kukidhi ubora.
Akizungumza wakati wa zoezi la uteketezaji wa bidhaa hizo zikiwemo vipodozi, vyakula na vinywaji, Kaimu Mkuu wa Kanda ya Kati ya Shirika hilo Bi. Salome Emmanuel amesema kuwa baadhi ya bidhaa zilizoteketezwa ni zile ambazo muda wake wa matumizi umekwisha na bado wafanyabiashara wasio waadilifu walikuwa wakiendelea kuziuza.
“Ukaguzi tuliofanya kati ya mwezi Oktoba na Desemba 2019 katika mikoa ya Dodoma na Singida umetuwezesha kubaini bidhaa hizi ambazo baadhi ya bidhaa zizisokidhi viwango na nyingine muda wake wa matumizi umekwisha lakini bado wafanyabiashara wasio waaminifu wamekuwa wakiendelea kuziuza” alisisitiza Bi. Solome
Akifafanua Bi. Solome amesema kuwa Shirika hilo litaendelea kufanya ukaguzi mara kwa mara ili kuhakikisha kuwa bidhaa zilizopo sokoni zinakidhi vigezo kwa mujibu wa sheria.
Aliongeza kuwa wananchi wana jukumu la kushirikiana na shirika hilo katika kuhakikisha kuwa wafanyabiashara wasio waadilifu hawafanikiwi kuuza bidhaa ambazo muda wake umekwisha na ambazo hazikidhi vigezo.
Aidha, aliwataka wafanyabiashara wote kuzingatia sheria na kanuni pale wanapotaka kuingiza bidhaa hapa nchini na hata wale wanaofanya uzalishaji hapa nchini.
Kwa upande wake mkaguzi wa Chakula wa Shirika hilo Bw. Abel Deule amesema kuwa Shirika hilo linaendelea kuhakikisha kuwa wananchi wanalindwa dhidi ya bidhaa zisizo na ubora na zile ambazo muda wake wa matumizi.
Shirika la Viwango Tanzania (TBS) limekuwa likifanya ukaguzi wa mara kwa mara ili kuhakikisha kuwa bidhaa zinazoingia nchini zinakidhi vigezo .
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...