Naibu Waziri wa Ujenzi, Eias
Kwandikwa, akiwasilisha taarifa ya utekelezaji ya Wakala wa Barabara
Tanzania (TANROADS), mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu,
jijini Dodoma.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi,
uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi), Arch. Elius Mwakalinga,
akifafanua jambo kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu, jijini
Dodoma, wakati Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), ulipowasilisha
Taarifa yake ya utekelezaji mbele ya Kamati hiyo.
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya
Bunge ya Miundombinu, Mhe. Selemani Kakoso (wa pili kulia), akitoa
maelekezo kwa Viongozi wa Wizara na watendaji wa Wakala wa Barabara
Tanzania (TANROADS), wakati Wakala huo ulipowasilisha Taarifa yake ya
utekelezaji mbele ya Kamati hiyo.
Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya
Bunge ya Miundombinu, wakimsikiliza Naibu Waziri wa Ujenzi, Eias
Kwandikwa (hayupo pichani), wakati akiwasilisha taarifa ya utekelezaji
ya Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), mbele ya Kamati ya Kudumu ya
Bunge ya Miundombinu, jijini Dodoma.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi,
uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi), Arch. Elius Mwakalinga,
akitoa maelekezo kwa watumishi wa Wizara yake wakati akikagua mafunzo ya
mfumo wa kielektroniki wa ufuatiliaji wa upimaji wa magari katika
mizani nchini.
…………………………………………
Serikali kupitia Wizara ya
Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi) imeanzisha utaratibu
wa kufuatilia utendaji kazi wa mizani kwa saa ishirini na nne kwa
kutumia mfumo wa kielektroniki na kamera za CCTV ili kuongeza uwazi na
uwajibikaji katika utendaji kazi wa mizani hizo na kudhibiti vitendo vya
rushwa.
Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa
Ujenzi, Elias Kwandikwa wakati akiwasilisha taarifa ya utekelezaji ya
wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) mbele ya Kamati ya Kudumu ya
Bunge ya Miundombinu jijini, Dodoma.
“Mfumo huu umetuwezesha kugundua
mwenendo mzima wa upimaji magari katika mizani kwani hata kama kuna
vitendo vya rusha vimefanyika, basi mfumo unatusaidia kubaini vitendo
hivi na inakuwa rahisi kuchukua hatua kwa yule aliyehusika”, amesema
Naibu Waziri Kwandika.
Aidha, amefafanua kupitia mfumo
huo suala la utunzanji wa barabara kupitia mpango wa udhibiti magari
yaliyozidisha uzito nalo ni la uhakika kwani magari yaliyozidisha uzito
yanaweza kubainika na kuchukuliwa hatua.
“Mathalani, katika kipindi cha
kuanzia Julai hadi Desemba 2019, jumla ya magari 3,080,285 yalipimwa
ambapo kati ya hayo, magari 19,432 yalikuwa yamezidisha uzito wa zaidi
ya asilimia tano ya uzito unaoruhusiwa na kutozwa tozo ya uharibifu wa
Barabara ambayo ni sawa na asilimia 0.63% ya magari yote yaliyopimwa”,
amesema Naibu Waziri.
Ameongeza kuwa Wizara inaendelea
kuelimisha wasafirishaji na wadau wengine kuhusu Sheria mpya ya Udhibiti
Uzito wa Magari ya Afrika Mashariki ya mwaka 2016.
Kwandikwa ameeleza kuwa katika
kuhakikisha Wakala unaendelea kusimamia kazi za udhibiti wa Uzito wa
magari umeendelea kuweka mfumo wa kupima magari yakiwa kwenye mwendo
ambapo kwa sasa mfumo huu tayari unafanya kazi katika vituo 13 na hivyo
kupunguza msongamano wa magari katika mizani pamoja na muda wa kusafiri.
Naibu Waziri Kwandikwa ametaja
kuwa baadhi ya vituo vya mizani vilivyofungwa mfumo huu ni pamoja na
Njuki (Singida), Nala (Dodoma), Wenda (Iringa) na Mpemba (Songwe).
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu Mhe. Selemani Kakoso,
ameupongeza Wakala huo kuendelea kutekeleza miradi yake ambayo ina tija
kwa Taifa na kusisitiza Wizara kuendelea kulipa madeni ya wakandarasi
ili kuwezesha miradi mingine ambayo imesimama kuendelea kutekelezwa.
“Naomba Wizara muendelee kulipa
madeni ya wakandarasi kwa kadri mnavyopata fedha kutoka Hazina,
mkichelewa kulipa mnasababisha miradi kukwama na wananchi kukosa
maendeleo”, amesema Mhe. Mwenyekiti
Katika hatua nyingine, Serikali
kupitia Wizara hiyo imeamua kununua gari maalum litakalogharimu kiasi
cha shilingi bilioni 1.2 kwa ajili ya ukaguzi wa barabara.
Gari hilo ambalo litakuwa la
kisasa litaweza kukagua mtandao wote wa barabara kuu hapa nchini ndani
ya mwezi mmoja na kutoa majibu ya ubora na mapungufu ya barabara kuanzia
hatua za awali za ujenzi hadi mradi utakapokamilika.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi,
Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi) Arch. Elius Mwakalinga, awali
wakati akikagua mafunzo ya mfumo kwa watumishi wa Wizara, unaoonesha
magari yanayopita kwenye mizani zote nchini na yale yanayozidisha uzito
barabarani, amesema kuwa mfumo huo sio wa kuviziana au kutafuta mchawi
au kuoneana wivu ila utasaidia kudhibiti wafanyakazi wa mizani na
wasafirishaji wanaocheza na mizani hizo.
Amesema kuwa mfumo huo una lengo
la kulinda miundombinu ya Taifa hususan barabara ili zisiendelee
kuharibiwa pia utarahisisha kuona kila fedha inayotozwa kwa
wasafirishaji.
“Mfumo huu ni wa kisasa na
umeshaanza kutuletea majibu kwa kuwabaini wale watoa rushwa na wala
rushwa katika mizani zetu hapa nchini”, amesisitiza Katibu Mkuu
Mwakalinga.
Arch. Mwakalinga ametoa wito kwa
wasafirishaji wote nchini kuhakikisha wanakuwa wazalendo na wanalinda
miundombinu ya barabara kwa kutokuzidisha uzito wa mizigo na bidhaa
wanayoibeba.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...