ILANI
ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) imetoa maelekezo kwa Serikali ya Jamuhuri
ya Muungano wa Tanzania (SMT) na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
(SMZ) kutekeleza miradi mbalimbali kwa lengo la kuboresha maendeleo ya
wananchi wake.
Ziara
ya siku nne ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim
Majaliwa kwenye Visiwa vya Unguja na Pemba kuanzia tarehe 17 hadi 20
Januari, 2020 ilikuwa na lengo la kuhakikisha ilani inatekelezwa kwa vitendo.
Ziara
hiyo ambayo ililenga kufuatilia utekelezaji wa maelekezo ya Ilani ya
uchaguzi ya mwaka 2015 – 2020 ni sehemu ya utaratibu wa kawaida wa
Waziri Mkuu kutembelea mikoa yote ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Waziri
Mkuu alikagua shughuli mbalimbali hususan utekelezaji wa miradi ya
maendeleo katika mikoa ya Kusini Unguja, Mjini Magharibi na Kaskazini
Unguja. Kwa upande wa Pemba alitembelea miradi mbalimbali ya maendeleo
katika mikoa ya Kusini Pemba na Kaskazini Pemba.
Mbali
na kuzungumza na watumishi, kusalimia wananchi pamoja na kupata
mrejesho kuhusu kero na malalamiko yao, pia Waziri Mkuu, alisisitiza
umuhimu wa watumishi wa umma kufuatilia makusanyo ya mapato na kudhibiti
matumizi ya fedha za walipa kodi.
MAPATO
Katika
Suala la mapato, Waziri Mkuu alisisitiza kuwa Serikali zote mbili (SMT
na SMZ) zipo makini na matumizi ya fedha zinazotokana na kodi za
wananchi, hivyo mtumishi yeyote atakayebainika kujihusisha na ubadhirifu
wa mapato ya Serikali hatoonewa haya.
Waziri
Mkuu alisema ili Taifa lolote liweze kupata maendeleo ni vema matumizi
sahihi ya fedha za walipa kodi yakasimamiwa ipasavyo. Alisisitiza kuwa
viongozi hawanabudi kutambua kuwa Serikali zote mbili za Muungano na
Zanzibar zipo makini na matumizi ya fedha hizo.
Aidha,
akiwa katika mkoa wa Kusini Unguja, Waziri Mkuu aliwaagiza wakuu wote
wa mikoa na wilaya wahakikishe wanachukua hatua kali kwa watumishi wa
umma ambao hawatekelezi majukumu yao ipasavyo, pamoja na watakaobainika
kufanya ubadhirifu wa fedha za umma.
Pia
aliwataka watumishi wa umma wasimamie vizuri ukusanyaji wa mapato na
wahakikishe fedha zote zinazopatikana zinaingizwa kwenye mfuko wa
Serikali. “Ni muhimu kwa watumishi kushirikiana katika ukusanyaji wa
mapato ili Serikali iweze kupata fedha za kugharamia miradi ya
maendeleo.”
Alisema
ni vema wakasimamia makadirio ya ukusanyaji wa mapato na wahakikishe
wanabaini vyanzo vyote na wafuatilie iwapo makadirio hayo ni sahihi na
fedha zote zinazokusanywa kama zinaingia katika mfuko mkuu wa Serikali.
Aliongeza kuwa makusanyo yafanyike kielektroniki.
KIWANDA CHA SUKARI CHA ZANZIBAR
Waziri
Mkuu alitembelea Kiwanda cha Sukari cha Zanzibar kilichopo eneo la
Mahonda kwa lengo la kujionea shughuli za uzalishaji kiwandani hapo,
ambapo alipokea malalamiko ya kukosekana kwa soko la sukari
inayozalishwa kiwandani hapo na ardhi ya kutosha kuongeza kilimo cha
miwa kutoka kwa mwekezaji Bw. Rahim Bhaloo.
Mwekezaji
huyo, alidai kuwa licha ya mahitaji ya tani 36,000 za sukari kwa upande
wa Zanzibar, anashindwa kupata soko la tani 6,000 anazozalisha
kiwandani hapo, ambapo Waziri Mkuu alimwelekeza Katibu Mkuu, Wizara ya
Biashara na Viwanda Zanzibar kuratibu vizuri utoaji wa vibali vya sukari
kutoka nje ili kuhakikisha sukari yote inayozalishwa na mwekezaji
inanunuliwa.
Waziri
Mkuu, alisisitiza umuhimu wa kulinda wawekezaji wa ndani na akasisitiza
kuhusu kufanya kazi pamoja baina ya Serikali na muwekezaji ili kukuza
ajira na soko la huduma.
Alimtaka
Mkuu wa mkoa Kaskazini Unguja, kuhamasisha wananchi kulima miwa kwa
kuwa soko la uhakika lipo na Halmashauri ya Wilaya ya Kati ione
uwezekano wa kupata ardhi kwa ajili ya mwekezaji kuongeza uzalishaji.
“Wizara
ya Viwanda lazima mbadilike na muweke utaratibu mzuri wa kusimamia
uingizwaji wa sukari kutoka nje. Haiwezekani sukari inayozalishwa ndani
ikakosa soko kutokana na uingizwaji wa sukari kutoka nje. Hatuwezi
kumfurahisha mtu mmoja huku wengi wakiumia.”
Waziri
Mkuu alisema Serikali imeamua kukuza uchumi kwa kupitia sekta ya
viwanda hivyo ni lazima viwanda vya ndani vikalindwa. “Viwanda
vinasaidia katika kuondoa tatizo la ajira, vinawapa wakulima soko la
uhakika la mazao yao pamoja na Serikali kupata kodi ya uhakika.”
Waziri
Mkuu alisema “haiwezekani sukari inayotengezwa na kiwanda hicho ambayo
ubora wake umethibitishwa na Shirika la Viwango Zanzibar ikakosa soko
hii haiwezekani tukashindwa kununua tani 6,000 huku mahitaji yetu ni
tani 36,000.”
Alisema
sera ya nchi inasisitiza umuhimu wa kulinda wazalishaji wa ndani ambao
bidhaa zao zimethibitishwa na mamlaka husika. Hivyo, ni lazima kuwalinda
wawekezaji kwa kuhakikisha wanapata masoko ya uhakika pamoja na
kuhamasisha wananchi kutumia bidhaa hizo.
Awali,Mkurugenzi
Mkaazi wa kiwanda cha Sukari Zanzibar, Bw. Rahim Bhaloo alisema kiwanda
chao kinazalisha tani 6,000 kwa mwaka huku kikiwa na uwezo wa kuzalisha
tani zaidi ya 20,000 kwa mwaka ila tatizo ni soko pamoja na ardhi ya
kutosha kulima miwa.
Alisema
kutokana na uhaba wa soko sukari waliyozalisha katika msimu wa mwaka
2019/2020 wameuza tani 2,800 tu na kiasi cha tani 3,200 bado kipo
kiwandani hapo, hivyo ameiomba Serikali iwasaidie kwa kuwatafutia masoko
pamoja na ardhi ili waweze kuongeza uzalishaji.
Mkurugenzi
huyo aliiomba Serika iwe inazuia utoaji wa vibali vya uagizaji wa
sukari kutoka nje hususani kipindi cha uzalishaji ili waweze kuuza
sukari yao na itakapoisha ndio vibali hivyo vianze kutolewa. Kiwanda
kimeajiri wafanyakazi 300, pia wakulima wa nje zaidi ya 800 wanauza miwa
yao kiwandani hapo.
Kwa upande wake,
Katibu Mkuu wa Wizara ya Biashara na Viwanda Zanzibar, Bw. Juma Hassan
Reli amemhakikishia Waziri Mkuu kwamba sukari yote iliyopo kiwandani
hapo itakuwa imeshanunuliwa ifikapo Februari mwaka huu. Pia maelekezo
yote aliyoyatoa kuhusu utoaji wa vibali vya uagizaji wa sukari
watayafanyia kazi.
AFYA
Waziri
Mkuu alitembelea Kituo cha Afya cha Kizimkazi, Dimbani kilichopo katika
Halmashauri ya Wilaya Kusini ambayo ilikuwa ni siku ya Afya ya Kijiji,
ambapo alizindua mashine ya ultra sound, kukagua huduma za afya
zilizokuwa zikitolewa ikiwemo upimaji wa afya kwa magonjwa ya shinikizo
la damu, meno, macho, uzito pamoja na homa ya ini. Vilevile, aligawa
vyandarua kwa akina mama wawili wajawazito kwa niaba ya wenzao 10.
Waziri
Mkuu aliwataka wajawazito aliowakabidhi vyandarua pamoja na wananchi
wengine wavitumie kujikinga na mbu na si kwa matumizi mengine tofauti kwa kuwa Serikali imegharamia vyandarua hivyo kwa fedha nyingi.
Pia,
Waziri Mkuu alizindua jengo la huduma ya mama na mtoto (yaani Kituo cha
Uzazi - Bambi) kilichopo katika Mkoa wa Kusini Unguja, ambapo
aliipongeza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa hatua mbalimbali
ilizochukua katika kuboresha huduma za afya.
Waziri
Mkuu alitumia fursa hiyo kuwasisitiza wananchi watumie vituo vyote vya
afya kwa ajili ya kupima na kutambua afya zao. Aliongeza kuwa ujenzi wa
kituo hicho ni sehemu ya jitihada kubwa inayofanywa na Serikali zote
mbili kwa lengo la kupunguza vifo vya mama na mtoto.
Waziri
Mkuu amewataka watumishi wa Sekta ya Afya waimarishe utoaji wa huduma
hizo kwa wananchi kwa sababu Serikali imefanya mabadiliko kwenye sekta
hiyo ikiwa ni pamoja na kuongeza bajeti ya dawa. Katika
kukabiliana na uchache wa watumishi katika Sekta ya Afya, Serikali ya
SMZ tayari imeajiri watumishi wapya 150 hivi karibuni.
ELIMU
Waziri
Mkuu alikagua ujenzi wa Kituo cha Mafunzo ya masomo ya Sayansi
kilichopo katika Jimbo la Paje-Unguja ambapo alisema ameridhishwa na
ujenzi wa mradi huo ambapo utakapokamilika utasaidia katika kupunguza
changamoto ya walimu wa kufundisha masomo ya sayansi.
Alisema
kuwa walimu wa masomo ya sayansi ni changamoto kubwa nchi nzima, hivyo,
Serikali zote mbili zinaendelea kuchukua hatua mbalimbali ili
kukabiliana na tatizo hilo. Hatua hizo ni pamoja na ujenzi wa vituo vya
aina hiyo 22 kwa upande wa SMZ.
“Mkakati
wa kuboresha mafunzo ya sayansi ni sehemu ya kupata wataalamu kwa ajili
ya kuifikia ndoto ya Tanzania ya uchumi wa viwanda, hivyo alimtaka
Katibu Mkuu, Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar ahakikishe
ujenzi huo unakamilika kwa wakati kama ilivyopangwa ifikapo tarehe 31
Machi 2020.
Akiwa kisiwani Pemba Waziri Mkuu alikagua maendeleo ya ujenzi wa chuo cha Mafunzo ya Amali cha Daya kilichopo Mtambwe wilaya ya Wete, Kaskazini Pemba, ambapo aliwaagiza Wakuu wa Mikoa na Wilaya nchini wasimamie ipasavyo suala la elimu hususani kwa watoto wa kike.
“Hakikisheni elimu kwa mtoto wa kike inasimamiwa vizuri na kuchukua hatua kwa watakaowakatisha masomo.Pia, Waziri Mkuu aliwataka Watoto wa kike watoe taarifa za watu wanaotaka kuwakatisha masomo yao kwa viongozi wa shehiya (vijiji) waliopo kwenye maeneo yao.
Waziri
Mkuu alisema Serikali imedhamiria kuwalinda watoto wa kike lengo likiwa
ni kuhakikisha wanamaliza masomo yao na hatimaye waweze kujikwamua wao
pamoja na familia zao. “Wanafunzi wa kike hakikisha mtu yeyote
atakayekugusa, kukufuatilia nenda kamshtaki kwa kiongozi wa Shehiya
husika. Vijana jihadharini na watoto wa shule ukikutwa naye jela miaka
30.”
Akizungumzia kuhusu taarifa za ufaulu hali ya ufaulu, Waziri Mkuu alionesha kutoridhishwa kwa Kiwango cha ufaulu hususan wa Elimu ya msingi,
hivyo, ameuagiza uongozi wa Wizara ya Elimu uhakikishe unafanya
mabadiliko katika kuisimamia sekta hiyo. “Maafisa elimu waache kukaa
maofisini waende mashuleni kusimamia ufundishaji.”
Alisema
Serikali inataka kuona watoto wakifanya vizuri kuanzia ngazi ya elimu
ya msingi hadi elimu ya juu. “Ili malengo hayo yatimie ni lazima
watendaji katika sekta ya elimu wakabadilika na kusimamia vizuri
ufundishwaji. Tunataka watoto wanapoanza masomo yao ya msingi wafike
hadi ngazi ya chuo kikuu ili tuwe na wataalamu wengi.”
Pia Waziri
Mkuu alitembelea Chuo cha kilimo cha Kizimbani ambacho kimepandishwa
hadhi na kuwa chuo kikuu kishiriki cha SUZA. Hata hivyo uongozi wa chuo
hicho ulimueleza kwamba chuo kinakabiliwa na changamoto ya kukosekana
kwa hati ya umiliki wa eneo la Makuyuni lililopo Bagamoyo ambapo
Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ililitoa kwa Chuo cha Kilimo
cha Kizimbani.
Akizungumza
na wanafunzi na wananchi chuoni hapo Waziri Mkuu alisisitiza umuhimu wa
kujifunza kwa bidii na kujenga dhana ya kujiajiri hususan katika kilimo
badala ya kutegemea ajira chache zinazotoka Serikalini. Pia, Waziri
Mkuu aliiagiza Wizara ya Kilimo na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali
Zanzibar zishirikiane na wenzao wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
kumaliza changamoto ya umiliki wa eneo la Makuyuni, Bagamoyo.
“Wizara
ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar ishirikiane na Wizara ya Elimu,
Sayansi na Teknolojia kutatua changamoto ya wahadhiri chuoni hapa na
Katibu Mkuu, Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar atenge bajeti
kwa ajili ya kuimarisha miundombinu ya chuo sambamba na kununua matrekta
kwa ajili ya mafunzo ya amali.”
Kadhalika, Waziri
Mkuu aliweka jiwe la msingi katika mradi wa maji wa Mwera samabamba na
kukagua chanzo cha maji na nishati ya umeme wa jua itakayotumika
kuendesha mradi huo, ambapo alimpongeza mwakilishi wa jimbo la Mwera,
Mheshimiwa Mihayo kwa kuchangia ujenzi wa mradi huo.
Akiongea
na wananchi wa Mwera, Waziri Mkuu alielekeza kuwa Halmashauri ziunge
mkono juhudi hizo kwa kutafuta fedha za kukamilisha mradi na kuibua
miradi mingine. Mradi huo unahusisha ujenzi wa tanki la kuhifadhia maji
pamoja na usambazaji kwa wananchi.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...