Na Mwandishi Wetu
MASHIRIKA na Taasisi mbalimbali yameshauriwa kuwapa kipaumbele wanawake kwenye nafasi za ajira kwani wamethibitisha kwamba wakipewa nafasi wanauwezo wa kuleta mabadiliko.
Hayo yamesemwa na Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu ARDHI (Taaluma), Profesa Gabriel Kassenga, wakati wa kongamano la siku ya wanawake duniani lililoandaliwa na wanawake wa chuo hicho.
Amesema, wanawake wengi waliopewa nafasi za uongozi wamefanyakazi kubwa hivyo kuondoa dhana iliyokuwepo kwamba hawana uwezo kama wanaume wakipewa nafasi kwani asilimia 70 ya wafanyakazi wa chuo hicho ni wanawake na wote wameonyesha uwezo mkubwa sana kwenye nafasi zao tofauti kabisa na dhana iliyokuwepo.
“Ile dhana kwamba wanawake hawana uwezo kama wanaume imepitwa na wakati kwa hiyo inapotokea nafasi za ajira wanawake wapewe kipaumbele kwasababu hapa kwetu wametuonyesha kwa vitendo kwamba wakipewa nafasi uwezo wanao,” amesema Profesa Gabriel.
Amesema ARU ina idara 13 za kitaaluma na kati ya hizo, idara nane zinaongozwa na wanawake na chuo kinaridhishwa na namna wanavyochapa kazi na kuleta matokeo makubwa kwenye idara wanazoongoza.
Kwa upande wake, Mkuu wa Kitengo cha Jinsia chuoni hapo, Dk. Nelly Babere, amesema lengo la kufanya kongamano hilo ni kuonyesha nafasi ya mwanamke katika maendeleo na katika jamii ya Chuo Kikuu ARDHI na kwamba chuo hicho kimejitahidi kuweka usawa wa kijinsia.
"Chuo kimejitahidi kuweka usawa wa wanawake kwenye nafasi mbalimbali za uongozi, uamuzi wowote unaofanywa unakuwa hauna ubaguzi, mambo mengi tunayofanya hapa ni shiriishi na hata wanafunzi huwa tunawashirikisha na kwenye maandamano ya leo kuadhimisha siku ya wanawake wanafunzi wameshirikishwa ili nao wajifunze usawa wa kijinsia,” amesema.
Dk. Nelly ameongeza kuwa, idadi ya wanafunzi wa kike ilikuwa ndogo sana wakati chuo hicho kinaanza lakini kwa sasa idadi yao imekuwa ikiongezeka mwaka hadi mwaka kiasi cha kuwa sawa na idadi ya wavulana kwani wakati chuo kinaanza miaka ya 2000 ulikuwa unakuta darasa zima linawanafunzi wakike wawili tu, lakini leo hii ukiangalia darasa lingine unakuta idadi ya wasichana ni kubwa kuliko wavulana.
Aidha ametoa wito kwa wanafunzi wa kike na wa kiume kujitambua kwani wamekuwa wakikabiliana na changamoto yofauti tofauti hivyo wajijielewa watavuka changamoto zinazowakabili.
Amesema ARU inashirikisha na jamii, serikali na jumuiya ya kimataifa kuendelea kuangalia nafasi ya mwanamke na kumlinda dhidi ya vitendo vya unyanyasaji ili aishi maisha ya staha na kuondokana na unyanyasaji na ukatili.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...