Mafundi kutoka Kampuni ya Stem ya Jijini Dar es Salaam wakiendelea na ujenzi wa sehemu ya mzunguko katika barabara ya Vigwaza hadi Bandari Kavu ya Kwala Mkoani Pwani.


Katibu Mkuu wa Uchukuzi, Gabriel Migire akimsikiliza Mhandishi Jacob Mambo kutoka wakala wa Barabara nchini(TANROADS) kuhusu ujenzi wa Barabara ya Zege Kutoka Vigwaza Mpaka Bandari Kavu ya Kwala wakati Katibu Mkuu huyo alipotembelea mradi huo Mkoani Pwani.




Katibu Mkuu wa Uchukuzi Gabriel Migire akitoa maelekezo kwa Watendaji wa Wakala wa Barabara Nchini (TANROADS) na SUMA JKT, wakati alipokagua maendeleo ya ujenzi wa Barabara yenye kiwango cha Zege kutoka Vigwaza mpaka Bandari Kavu ya Kwala Mkoani Pwani.



Muonekano wa hatua iliyofikiwa ya ujenzi wa Barabara ya Zege kutoka Vigwaza Mpaka Bandari kavu ya Kwala, Mkoani Pwani ambapo ujenzi huo umefikia asilimia 95, na inatarajiwa kuanza kutumika mwanzoni mwa mwaka 2023.



Katibu Mkuu wa Uchukuzi, Gabriel Migire (kulia) akimsikiliza Mhandisi Joseph Marandu kutoka SUMA JKT kuhusu hatua ya Ujenzi wa Bandari Kavu ya Kwala, wakati Katibu Mkuu huyo alipokagua mradi huo, Mkoani Pwani.

PICHA NA WUU



Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi (Sekta ya Uchukuzi), Bw. Gabriel Migire amesema kufikia Januari, 2023 Bandari kavu ya Kwala iliyopo Mkoani Pwani itaanza kuhudumia mizigo itakayotoka Bandari ya Dar es Salaam na kuelekea mikoa mbalimbali nchini na nchi jirani.

Katibu Mkuu Migire ameyasema hayo wakati alipokagua ujenzi wa barabara yenye urefu wa kilometa 15 kutoka Vigwaza mpaka Bandari Kavu ya Kwala inayojengwa kwa kiwango cha zege na Kampuni ya Stem kutoka Jijini Dar es Salaam na kusisitiza kuwa Serikali itaendelea kuhakikisha utendaji wa bandari unaboreshwa ili kuvutia wateja wengi zaidi.

“Kuanza kutumika kwa Bandari hii ya Kwala itasaidia kupunguza msongamano wa mizigo na magari makubwa katika Bandari ya Dar es Salaam kwani bandari hii itahifadhi makasha ya kwenda nchi Jirani kama vile Burundi, Rwanda, DRC Congo, Uganda , Zambia na Malawi”, amesisitiza Bw. Migire.

Kwa upande wake, Mhandisi Joseph Marandu kutoka SUMA JKT anayesimamia ujenzi wa Bandari ya Kwala amesema kuwa ujenzi mradi wa barabara hiyo utakamilika mwishoni mwa mwezi huu na kazi zilizoendelea kutekelezwa kwa sasa ni za uwekaji wa taa, kamera pamoja na kumalizia kuweka sakafu ngumu kwa ajili ya kuhifadhia makasha.

Naye, Mhandisi Jacob Mambo kutoka Wakala wa Barabara Nchini (TANROADS), amesema katika utekelezaji wa mradi huo mradi umezingatia mzigo mkubwa utakapohifadhiwa kutoka bandarini hivyo wakala umehakikishia unakamilika kwa viwango..

Mradi wa Ujenzi wa Bandari ya Kavu ya Kwala unategemewa kupunguza kwa kiasi kikubwa foleni ya malori katika Bandari ya Dar es Salaam na utarahisisha utendaji wa bandari hiyo kwani mizigo itaweza kushushwa kwenye meli na kupelekwa kwenye bandari hiyo kavu.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...