Na Wankyo Gati, ARUSHA
UPANDE wa Jamuhuri umeiomba Mahakama ya Hakimu Mkazi ya jijini Arusha kuiondoa
kesi ya kujifanya Afisa usalama wa Taifa na kujipatia chakula katika hotel moja ya kimataifa jijini Arusha inayomkabili aliyekuwa Mwenyekiti wa UVCCM Mkoa huo Bw.
Lengai ole Sabaya.
Akitoa ombi hilo Wakili wa Serikali Bi. Grace Madikenya mbele ya Hakimu wa
Mahakama ya Hakimu mkazi Arusha, Mhe. Gwantwa Mwakuga, alisema upande wa
Jamhuri hauna nia ya kuendelea na kesi hiyo sababu shahidi mmoja
muhimu yupo nje ya nchi kwa miezi 18.
“Sasa tumeona tutamtesa mteja wetu. Hivyo kwa nia njema kabisa
tumeamua kuiondoa mahakamani kesi hii, maana miezi hii 18 ni mwaka mmoja
na miezi sita,”alisema.
Ombi hilo lilipingwa vikali na Wakili wa utetezi, Bi. Edna Haraka na
kuiomba mahakama hiyo iendelee na kesi hiyo, kwa madai kuwa upande wa mwendesha
mashitaka unatumia Mahakama kama kichaka cha kumnyima haki mteja wao
na kumnyanyasa.
Alisema upande huo hauna nia njema na mshitakiwa na kwamba kitendo cha kuiondoa kesi
hiyo mahakamani sio mara ya kwanza ni mara ya pili, ambapo ya kwanza
waliomba hivyo na mahakama ilipofuta walimkamata mteja wao na kumnyima
dhamana.
“Sasa leo tupo katika kusikiliza shahidi wa tatu na badala ya kuleta
shahidi walileta maelezo ya shahidi na leo wanakuja na stori ya kuiondoa ili waendelee kumyanyasa mteja wetu. Hapana! Ofisi hiyo ya Mwanasheria Mkuu inatumika vibaya kwa kivuli cha Mahakama,”alisema
Edna
Wakili huyo alisema serikali ya sasa inasisitiza mpango wa kuharakisha
mashauri kusikiliza wa BRN, sasa wakati inafanyika hivyo wengine wanachelewesha kwa sababu zao.
Hakimu Gwantwa Mwakuga baada ya kusikiliza pande zote mbili, alisema
atatoa uamuzi Aprili 28 mwaka huu, ya kama anakubali shauri liondolewe au
la. Bw. Lengai anakabiliwa na shitaka la kujifanya Afisa Usalama wa Taifa na kujipatia huduma ya chakula na malazi kwenye Hotel ya kimataifa ya Highway ya jijini Arusha.
Kutoka maktaba: Aliyekuwa Mwenyekiti wa UVCCM mkoa wa Arusha Bw. Lengai Ole Sabaya (katikati) na wakili wake na wakitoka mahakamani siku za nyuma.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...