Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Dkt. Kebwe Stephen Kebwe anamsikiliza Mgeni wake baada ya kumkabidhi kitabu kinachoonyesha maeneo ya Uwekezaji Mkoani Morogoro (Morogoro Region Investment Guide).

Na. Andrew Chimesela - Morogoro

Serikali ya Uingereza imeonesha nia ya kushawishi wawekezaji nchini mwake kuja kuwekeza hapa nchini hususan katika Mkoa wa Morogoro katika Sekta mbalimbali ikiwemo Sekta ya Kilimo, viwanda na Madini. Hayo yamefahamika jana Julai 18 mwaka huu wakati wa mazungumzo yaliyofanyika Ofisini kwa Mkuu wa Mkoa wa Morogoro baina ya Balozi wa Uingereza hapa nchini, Sarah Cooke na Dkt. Kebwe Stephen Kebwe Mkuu wa Mkoa huo.

Awali viongozi hao wawili walianza mazungumzo yao kuhusu miradi ya maendeleo inayofadhiliwa na Uingereza hapa nchini hususan iliyopo Mkoani Morogoro ikiwemo miradi ya Elimu - Educationa Programme for Results (EP forR), ambapo Mhe. Cooke alisema nchi yake imeongeza ufadhili wake kutoka 34% mwaka 2012 hadi 70/% mwaka 2016.
Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Dkt. Kebwe Stephen Kebwe akimkabidhi Balozi wa Uingereza hapa nchini, Sarah Cooke kitabu cha Uwekezaji.

Kwa upande wa Afya Balozi huyo alisema katika Mkoa wa Morogoro, Uingereza imefadhili Vituo vya Afya katika eneo linalolenga Mpango wa Uzazi kwa akina mama kupitia Mradi wa Population Service International (PSI) ambapo hadi sasa jummla ya akinamama 9,400 Mkoani humo wamefaidika na huduma hiyo.

Aidha, Viongozi hao wawili walizungumzia ufadhili unaotolewa na Uingereza katika nyanja za Maji na Usafi wa Mazingira ikiwemo Kampeni inayoendelea sasa Mkoani Morogoro ya usichukuliepoanyumbanichoo, Mkoa huo ukiwa ni Mkoa wa Majaribio katika Kampeni hiyo.

Pamoja na miradi mingine mingi waliyoizungumzia , Viongozi hao pia waligusia miradi ya Sekta ya Kilimo na Miundombinu. Kwa upande wa Sekta ya Miundombinu upo mradi wa IRAT yaani Improving Rural Access in Tanzania ambapo Uingereza imefadhili matengenezo ya makaravati ya barabara ya Chagongwe - Kumbulu iliyopo Wialaya ya Gairo.
Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Dkt. Kebwe Stephen Kebwe anamsindikiza mgeni wake, Balozi wa Uingereza hapa nchini, Sarah Cooke baada ya kukamilisha mazungumzo yao.

Baada ya kumaliza mazungumzo kuhusu miradi inayofadhiliwa na nchi ya Uingereza, Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Dkt. Kebwe Stephen Kebwe alimshukuru Balozi wa Uingereza kwa Ufadhili wa miradi yote hiyo ukiwemo mradi mkubwa wa Upimaji na umilikishaji wa Ardhi unaotekelezwa katika Wilaya za Kilombero, Ulanga na Malinyi kupitia Land Tenure Support Programme.

Dkt. Kebwe ametumia fursa hiyo kumweleza Balozi Sarah Cooke uwepo wa maeneo mazuri ya uwekezaji katika Mkoa wa Morogoro na akawasilisha ombi kwa balozi huyo kushawishi wawekezaji walioko nchini mwake kuja kuwekeza Mkoani Morogoro katika sekta mbalimbali ikiwemo ya Kilimo, viwanda na uchimbaji wa madini ya dhahabu na Graphite.

Balozi Sarah Cooke alionekana kushawishika na ombi la mwenyeji wake na kuahidi kulifanyia kazi haraka huku akiahidi kutafuta muda wa kufanya ziara katika Mkoa wa Morogoro kwa lengo la kutembelea miradi wanayoifadhili lakini pia kutembelea maeneo ya uwekezaji kama alivyokuwa ameombwa na mwenyeji wake.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...