Na Veronica Kazimoto,Geita

Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imewaelimisha wafanyabiashara na wadau mbalimbali walioshiriki Jukwaa la Fursa za Biashara mkoani Geita na kuwafafanulia juu ya masuala mbalimbali yanayohusu kodi ikiwa ni pamoja na msamaha wa riba na adhabu kwenye malimbikizo ya madeni ya kodi. 

Akizungumza wakati akiwasilisha mada kuhusu kodi katika jukwaa hilo, Mkurugenzi wa Huduma na Elimu kwa Mlipakodi wa mamlaka hiyo amewataka wafanyabiashara wenye malimbikizo ya madeni ya kodi na wale wote waliokuwa wakifanya biashara bila kusajiliwa kuchangamkia msamaha huo ipasavyo kwani hilo ni zoezi la miezi sita pekee.

"Nachukua fursa hii kutoa wito kwa wafanyabiashara wote wenye malimbikizo ya madeni ya kodi na wote waliokuwa wakifanya biashara bila kusajiliwa kuwasilisha maombi yao TRA ili waweze kupata msamaha huu wa riba na adhabu wa asilimia 100 ambapo mwisho wa kutuma maombi ni tarehe 30 Novemba, 2018. 

Aidha, Mkurugenzi Kayombo amewahimiza wafanyabiashara wadogo waliopo kwenye utaratibu wa makadirio kusajiliwa na kupatiwa Namba ya Utambulisho wa Mlipakodi (TIN) ambayo hutolewa na TRA bure bila ulazima wa kulipa kodi ya awamu ya kwanza kabla ya kuanza biashara isipokuwa ndani ya siku 90 baada ya kuanza biashara.

“Awali wafanyabiashara walikuwa wanalipa kodi mara tu baada kusajili biashara zao na kukadiriwa kodi, lakini sasa hivi tumeweka utaratibu wa kulipa kodi ndani ya siku 90 kwa awamu ya kwanza baada ya kusajiliwa na na kuanza biashara, alifafanua Kayombo.

Pamoja na mambo mengine, Kayombo amewakumbusha wafanyabiashara na washiriki wa jukwaa hilo la fursa za biashara suala zima la kutoa risiti za kielektroniki za EFD kila wanapouza bidhaa na huduma mbalimbali na kudai risti kila wanafanya manunuzi.

Vilevile, amewasisitiza wafanyabiashara wote wa Mkoa wa Geita na wilaya zake wenye changamoto mbalimbali wasisite kuonana na Meneja wa TRA mkoani humo kwa ajili ya kupata ufumbuzi wa changamoto zinazowakabili ili waweze kufanya biashara zao kwa uhuru.

Jukwaa la Fursa za Biashara limeandaliwa na Ofisi ya Mkoa wa Geita kwa kushirikiana na Shirika la Magazeti ya Serikali (TSN) ambapo Mamlaka ya Mapato Tanzania imeshiriki jukwaa hilo kwa ajili ya kutoa elimu ya kodi kwa wafanyabiashara na wadau mbalimbali hususani wa mkoani hapa. 
Mkurugenzi wa Huduma na Elimu kwa Mlipakodi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Richard Kayombo akiwasilisha mada kuhusu kodi wakati wa Jukwaa la Fursa za Biashara linalomalizika leo mkoani Geita likiwa na lengo la kuibua fursa mbalimbali za uwekezaji zilizopo katika mkoa huo pamoja na changamoto mbalimbali kwa lengo la kupata ufumbuzi.
Mkurugenzi wa Huduma na Elimu kwa Mlipakodi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Richard Kayombo akiwasilisha mada kuhusu kodi wakati wa Jukwaa la Fursa za Biashara linalomalizika leo mkoani Geita likiwa na lengo la kuibua fursa mbalimbali za uwekezaji zilizopo katika mkoa huo pamoja na changamoto mbalimbali kwa lengo la kupata ufumbuzi.
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Dkt. Harrison Mwakyembe (aliyevaa kofia) akizungumza wakati alipotembelea banda la Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) wakati wa maonyesho yaliyoambatana na Jukwaa la Fursa za Biashara linalomalizika leo mkoani Geita kwa lengo la kuibua fursa mbalimbali za uwekezaji zilizopo katika mkoa huo pamoja na changamoto mbalimbali kwa lengo la kupata ufumbuzi.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...