Na Karama Kenyunko, blogu ya jamii
KADA wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Iringa, Michael Mlowe maarufu kwa jina la Mayko Namlowe (44) anayeishi Iringa eneo la Lugalo Kihesa leo Oktoba 10 2018 amefikishwa Mahakama ya hakimu Mkazi Kisutu.
Kada huyo wa CCM anakabiliwa na mashtaka ya kuishi nchini bila kibali na kutoa maelezo ya uongo.
Akisoma hati ya mashtaka Wakili wa Serikali kutoka Uhamiaji, Novatus Mlay amedai, mshtakiwa Namlowe ambaye pia ni mfanyabiashara anadaiwa kuwa Mei 31 mwaka 2018 katika Makao Makuu ya Ofisi ya Uhamiaji iliyopo wilayani Temeke akiwa raia wa Uingereza alikutwa akiishi nchini bila ya kuwa na Visa(hati ya kusafiria) ama nyaraka yoyote inayomwezesha kufanya hivyo.
Katika shtaka la pili la kutoa maelezo ya uongo, ambapo imedaiwa Mei 31, mwaka huu katika ofisi hizo za uhamiaji mshtakiwa alitoa maelezo ya uongo kuhusiana na uraia wake raia na kufanikiwa kujipatia kitambulisho cha uraia namba 19741219_51108_00001_24 ambacho kina jina la Michael Juma Mlowe wakati akijua alichokifanya ni kosa.
Hata hivyo, mshtakiwa amekana kutenda makosa hayo na hakimu Mmbando amemtaka mshtakiwa huyo kuwa na wadhamini wawili wanaoaminika wenye barua na vitambulisho.
Mshtakiwa huyo anayetetewa na Wakili Kashindye Thabiti amekamilisha masharti ya dhamana na kuachiwa huru.
Kwa mujibu wa upande wa mashtaka, upelelezi katika kesi hiyo bado haujakamilika.
Kada wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Iringa, Michael Mlowe maarufu kwa jina la Mayko Namlowe (44) akiingia katika mahakama ya hakimu mkazi jijini Dar es Salaam leo.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...