"MAHAKAMA"
Showing posts with label MAHAKAMA. Show all posts
MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam, imepiga marufuku kurushwa mubashara (live) kwa kesi ya uhaini inayomkabili Mwenyekiti wa Chadema, Tundu Lissu, katika hatua ya kusomewa maelezo ya mashahidi (committal proceedings).

Uamuzi huo umetolewa na Hakimu Mkazi Mfawidhi Franco Kiswaga, baada ya kukubaliana na ombi la upande wa Jamhuri ukiongozwa na Wakili wa Serikali Mkuu, Nassoro Katuga, uliolenga kulinda usalama na utambulisho wa mashahidi.

Hakimu Kiswaga alisema kuwa hatua hiyo haiwazuii wananchi wala mshtakiwa kusikiliza kesi hiyo, bali inalenga kuzuia kufichuliwa kwa mashahidi wa siri.

“Kuzuia kurushwa mubashara hakumzuii mshtakiwa kusikilizwa, bali kunazuia ueneaji unaoweza kuhatarisha usalama wa mashahidi,” alisema Hakimu Kiswaga.

Kwa mujibu wa amri hiyo, vyombo vya habari au watu binafsi wamekatazwa kuchapisha au kusambaza nyaraka zozote zinazoweza kufichua majina, anuani au taarifa binafsi za mashahidi, isipokuwa kwa ruhusa ya Mahakama.

Uamuzi huu unafuatia agizo la Mahakama Kuu la Agosti 4, 2025, lililotolewa na Jaji Hussein Mtembwa, lililobainisha kuwa mashahidi ambao ni raia lazima walindwe kwa kufichwa utambulisho wao, wakati wale ambao si raia watatoa ushahidi kwa utaratibu wa kawaida.

Baada ya amri hiyo kutolewa, maafisa wa Mahakama Kuu waliokuwa wakirusha mubashara kesi hiyo walilazimika kuzima kamera zao.

Lissu anakabiliwa na tuhuma za uhaini, ambapo inadaiwa Aprili 3, 2025 jijini Dar es Salaam, alitoa kauli zinazodaiwa kushawishi umma kuzuia kufanyika kwa Uchaguzi Mkuu wa Tanzania.
MAHAKAMA Kuu ya Masijala ya Dar es Salaam imekubali ombi la upande wa Jamhuri la kuficha majina na taarifa nyingine za mashahidi raia wa upande wa Mashitaka katika kesi ya uhaini inayomkabili Mwenyekiti wa Chadema, Tundu Lissu.

Akisoma uamuzi huo leo, Agosti 4, 2025, Jaji Hussein Mtembwa amesema kutokana na uzito wa kosa la uhaini na hofu ya mashahidi kutishiwa, ni haki kwa mashahidi raia kulindwa kwa kutotajwa majina yao, anuani wala mahali walipo katika hatua ya committal, Preliminary Inquiry (PI) na hata wakati wa kusikilizwa kwa kesi hiyo.

Jaji Mtembwa amesema kwa mujibu wa kiambatanisho kilichowasilishwa na upande wa mashtaka, kesi inayomkabili mshtakiwa katika Mahakama ya Kisutu inahusu uhaini. Akifafanua zaidi, amesema kwa kuwa mshtakiwa ana wafuasi wengi ndani na nje ya nchi, na kwa mujibu wa taarifa zilizowasilishwa na ACP Amini Mahamba kuwa mashahidi hao wanatishiwa na watu wa karibu na mshtakiwa ili wasitoe ushahidi mahakamani, usalama wao unaweza kuwa hatarini.

"Nilichokiona ni kwamba kosa la mshtakiwa ni kati ya makosa makubwa, na pili, mashahidi hawa wanaotarajiwa kwa kiapo cha ACP Mahamba ni kwamba wanatishiwa... Sisi kama Mahakama tukifikia hapo, tutaangalia Sheria inasemaje," amesema Jaji.

Ameongeza kuwa Sheria inaruhusu kuwalinda mashahidi na watoa taarifa, hasa pale ambapo wao au familia zao wako katika hatari ya kudhuriwa, ingawa pia inapaswa kuzingatiwa kuwa mshtakiwa ana haki ya kumuona na kumhoji shahidi.

"Mahakama ina wajibu wa kulinganisha haki zote mbili kwa uwiano kwa lengo la kutenda haki. Nimeamua kukubali maombi ya kuficha mashahidi ambao ni raia tu," amesema.

Hata hivyo, Mahakama imekataa ombi la Jamhuri la kuficha taarifa za mashahidi wote bila kujali uraia, na kueleza kuwa mashahidi ambao si raia wataendelea kutoa ushahidi kwa kawaida na kwa majina yao halisi.

"Kama shahidi si raia, atatoa ushahidi katika hali ya kawaida kwa kuonekana na bila kufichwa jina au taarifa nyingine zinazomhusu," amesema.

Aidha, Mahakama imeiagiza Ofisi ya Taifa ya Mashtaka kuandaa utaratibu wa kuchuja (screen) taarifa zote zitakazowasilishwa mahakamani ili kuondoa zile zinazoweza kufichua utambulisho wa mashahidi raia.

Pia, Mahakama imesema vyombo vya habari havitaruhusiwa kuchapisha au kutangaza taarifa yoyote inayoweza kufichua utambulisho wa mashahidi hao bila kibali cha Mahakama.

"Wakati wa committal, PI na hata wakati wa usikilizwaji, suala la kuchapisha au kusambaza taarifa zenye majina ya mashahidi wa upande wa mashtaka limepigwa marufuku. Haina maana unaficha mahakamani halafu chombo cha habari kinamtaja shahidi. Vyombo vya habari vitaruhusiwa kufanya hivyo tu kwa kupata kibali cha Mahakama," amesema.

Mahakama imekazia kuwa hairuhusiwi kusambaza au kuchapisha taarifa yoyote inayoweza kufichua jina, makazi, ndugu, marafiki au watu wa karibu wa mashahidi hao isipokuwa kwa ruhusa maalum kutoka kwa Mahakama.

Karama Kenyunko, Michuzi TV
UPANDE wa mashtaka katika kesi ya uhaini inayomkabili Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Tundu Lissu, umepewa hadi Juni 13, 2025, kuhakikisha unamsomea mshtakiwa huyo maelezo ya mashahidi (committal proceedings), ili kesi hiyo iweze kupelekwa Mahakama Kuu kwa ajili ya kuanza kusikilizwa.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Franco Kiswaga, alitoa agizo hilo leo, Julai 30, 2025, wakati shauri hilo lilipoitwa kwa ajili ya kutajwa na kusomwa kwa maelezo ya mashahidi pamoja na idadi ya vielelezo vitakavyotumika katika kesi hiyo.

Awali, Wakili wa Serikali, Nassoro Katuga aliiambia mahakama kuwa hawajawasilisha taarifa ya mashtaka Mahakama Kuu kwa kuwa waliwasilisha maombi ya kutaka kulinda taarifa za mashahidi, ambayo bado hayajatolewa uamuzi.

"Maombi hayo yenye namba 17059/2025 tayari yalisikilizwa Mahakama Kuu, na uamuzi wake unatarajiwa kutolewa Agosti 4, mwaka huu," alieleza Katuga.

Alifafanua kuwa, kwa kuwa maelezo ya mashahidi yanahusiana moja kwa moja na maombi hayo ya ulinzi, Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) ameshindwa kupeleka taarifa hiyo Mahakama Kuu hadi uamuzi wa maombi hayo utakapojulikana.

Hata hivyo, Lissu alipinga maelezo hayo akisema kuwa tayari mahakama ilishatoa amri kuwa ifikapo Julai 30, 2025 taarifa hiyo iwe imewasilishwa, jambo ambalo halijatekelezwa.

"Tunapoteza muda kwa ahirisho zisizo na msingi. Kama kweli mahakama hii ni huru, basi ikatae ahirisho hili. Kila mara wanakuja bila taarifa, ni matumizi mabaya ya mahakama na dharau kwa amri zako, mheshimiwa," alisema Lissu kwa msisitizo.

Aidha, aliongeza kuwa kukubali kila hoja ya upande wa mashtaka ni sawa na kuhalalisha njama za kunyimwa haki na kukandamiza haki za watu kwa kutumia taasisi za sheria.

Akihitimisha hoja hizo, Hakimu Kiswaga alisema kesi hiyo itaendelea Julai 13, 2025, akieleza kuwa hoja zimekuwa zikijirudia mara kwa mara na kwamba anahitaji muda wa kutafakari kabla ya kutoa uamuzi wa mwisho kuhusu hatua inayofuata.

Kwa mujibu wa hati ya mashtaka, Lissu anadaiwa kutenda kosa la uhaini Aprili 3, 2025, jijini Dar es Salaam. Inadaiwa kuwa alitoa kauli inayochochea uasi kwa kusema:

"Walisema msimamo huu unaashiria uasi, ni kweli kwa sababu tunasema tutazuia uchaguzi, tutahamasisha uasi, hiyo ndio namna ya kupata mabadiliko... kwa hiyo tunaenda kukinukisha sanasana huu uchaguzi tutaenda kuvuruga kwelikweli, tunaenda kukinukisha vibaya sana."

 



MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam imeahirisha kuanza kusikilizwa kwa kesi ya kuchapisha taarifa za uongo inayomkabili Mwenyekiti wa CHADEMA, Tundu Lissu kupisha usikilizwaji wa maombi ya Jamuhuri wanaoomba mashahidi wao kufichwa kipindi cha usikilizwaji wa kesi.

Uamuzi huo umetolewa leo Juni 2, 2025 na Hakimu Mwandamizi Geofrey Mhini baada ya kumaliza  kusikiliza maombi ya upande wa Jamuhuri ambao waliomba ahirisho la kesi ili maombi yao ya kutaka mashahidi wafichwe wakati wa usikilizwaji yasikilizwe na kutokewa uamuzi.

"Nakubaliana na upande wa mashtaka kwamba kuna sababu za msingi za kuahirish usikilizwaji wa kesi hii kupisha usikilizwaji wa maombi ya Jamuhuri hivyo naiahirisha kesi hii hadi Juni 16, 2025 itakapokuja kwa ajili ya kusikilizwa,". 

Akiwasilisha maombi hayo mapema leo Wakili Wa Serikali Mkuu, Nassoro Katuga amedai uamuzi utakaotolewa katika maombi hayo utawapatia mwangaza wa jinsi gani wataendelea na kesi hiyo. 

"Mheshimiwa kesi leo imekuja kwa ajili ya kuanza kusikilizwa lakini tunaleta maombi, tumefaili  maombi ya upande mmoja  chini ya kifungu cha sheria 188(1) cha kumlinda shahidi na kikiambatana na kifungu  392 (A) cha  Mwenendo wa Makosa ya Jinai (CPA),".

Akipinga hoja hizo Wakili wa Utetezi Peter Kibatala amedai upande wa Jamuhuri umeshindwa kutoa taarifa za kutosha kuiwezesha mahakama kuahirisha kesi hiyo kwa sababu hawajasema kama maombi hayo yanahusu mashahidi wote 15 pamoja na mambo mengine. 

Amesema mara ya mwisho walisema wana mashahidi 15 lakini je wote hao wanataka kufichwa? wangeleta mashahidi wengine basi, sidhani kama wenzetu wanania ya kuendelea na kesi hii.

Pamoja na mambo mengine, Wakili Kibatala amedai upande wa mashataka unataka kuficha mashahidi wao hasa mapolisi kwa sababu wanajua kuwa watakuja kuwagalagaza hapa mahakamani na haswa kwa sababu kesi inasikikizwa mubashara.

Kesi hiyo imeahirishwa hadi Juni 16, 2025 kwa ajili ya kuanza kusikilizwa kwa mashahidi wa Upande wa Jamuhuri 

Katika kesi hiyo ilidaiwa Aprili 3,2025
katika shtaka la kwanza Lissu alichapisha taarifa
inayosema "Uchaguzi wa serikali za mitaa 2024 wagombea wa CHADEMA walienguliwa kwa maelekezo ya Rais" wakati akijua sio kweli.
 
Katika shitaka la pili inadaiwa kuwa Aprili 3,2025 Lissu kupitia mtandao wa youtube alichapisha tarifa inayosema "Mapolisi wanatumika kuiba kura wakiwa na vibegi"
wakati akijua sio kweli.

Na shtaka la tatu  aliendelea kudai kuwa Lissu alichapisha tarifa ya uongo kwa nia ya kupotosha umma kupitia
mtandao wa youtube inayosema "Majaji ni ma-CCM hawawezi kutenda haki wapate teuzi na kuchaguliwa kuwa majaji wa mahakama ya rufaa" wakati akijua tarifa hiyo ni uongo na inapotosha umma.


HATIMAE wale, mwanafunzi watatu wanaodaiwa kumdhalilisha mwenzao ambae ni Mwanafunzi wa Chuo Kikuu Ardhi, Dar es Salaam Magnificat Kimario wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam kwa ajili ya kusomewa mashtaka yanayomkabili.

Wanafunzi hao kwa sasa wapo chini ya ulinzi wa Jeshi la Polisi wakisubiri kupandishwa kizimbani kutokana na video ya Aprili 20,2025 iliyozua mjadala mkubwa katika mitandao kijamii ikionesha wasichana wakigombana wakimuhusisha mtu mmoja aliyefahamika kwa jina la Mwijaku.

Kwa mujibu wa taarifa ya Jeshi la Polisi ya Aprili 24,2025 lilithibitisha kuwahoji wanafunzi hao ambao ni Mary Matogoro Mwanafunzi wa Chuo Kikuu Dar es Salaam, Ryner Mkwawili, Mwanafunzi wa Chuo Kikuu Ardhi, Dar es Salaam na Asha Juma Mwanafunzi wa Chuo cha Uhasibu, Dar es Salaam.

Pia, lilithibitisha kumuhoji Mwemba Burton Mwemba maarufu Mwijaku.

DALALI mmoja anayeishi Kipunguni jijini Dar es Salaam, Charles Shirima amefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu akikabiliwa na mashitaka 42 ikiwemo utakatishaji fedha kiasi cha Sh milioni mbili.

Mshitakiwa amesomewa mashtaka yake na wakili wa serikali Michael Shindai mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu Romuli Mbuya Aprili 6,2025

Shidai amedai kuwa mashtaka ya kwanza hadi ya tisa ni kuchapisha taarifa za uongo.

Inadaiwa kuwa kati Desemba 30,2024 maeneo yasiyojulikana,ndani ya jamhuri ya Muungano wa Tanzania mshtakiwa alichapisha taarifa za uongo katika mtandao wa kijamii wa Facebook kuwa TULIA TRUST FOUNDATION inatoa mkopo hadi milioni 50,000,000 huku akijua sikweli

Aliendelea kudai kuwa mashtaka ya 10 hadi 17 ni kujifanya mtu mwingine na kujitambulisha kwa watu mbalimbali.

Inadaiwa kuwa katika tarehe tofauti kati ya Desemba 31,2024 hadi Aprili 2025 ndani ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania mshitakiwa huyo akijitambulisha kwa David Sylvester Mugasa, Upendo Lawrence Kiwelu na wengine 6 kuwa yeye ni Spika wa Bunge Tulia Acksob Mwansasu

Wakili Shidai aliendelea kudai kuwa mashtaka 18 mpaka 37 nikujipatia fedha kwa njia ya udanyanyifu kutoka kwa watu mbalimbali ambapo inadaiwa kati ya Januari 31,2025 mshtakiwa huyo alijipatia kiasi cha Sh milioni mbili kupitia namba mbalimbali zilizosajiliwa majina ya watu tofauti tofauti zaidi ya 20 akidai kuwa angeawapatia mkopo huku akijua kuwa siyo kweli.

Katika mashtaka kuanzia 38 mpaka 41 mshtakiwa anakabiliwa na tuhuma za kutumia laini iliyosajiliwa kwa majina ya mtu mwingine bila ruhusa ya mtoa huduma.

Inadaiwa, kati April 29,2025 maeneo ya Kipunguni B Wilaya ya Ilala Mkoa wa Dar es salaam mshtakiwa alitumia namba za simu zilosajiliwa kwa watu wengine huku akijua kufaya hivyo ni kosa kisheria.

Katika shtaka la 42 la utakatishaji fedha, mshtakiwa anadaiwa kati ya Desemba 24,2024 hadi Aprili 2025 alijipatia kiasi cha Sh milioni 2, 827,000 huku akijua fedha hizo ni mazalia ya kosa tangulizi la kujipatia fedha kwa njia ya udanyanyifu.

Hata hivyo mshtakiwa hakuruhusiwa kujibu kitu chochote mahakamani hapo kwa kuwa kosa la utakatishaji fedha halina dhamana. Kwa mujibu wa upande wa Mashtaka upelelezi katika kesi hiyo bado unaendelea.

Kesi hiyo itatajwa tena Mei 22,Mwaka huu saa 4:00 asubuhi kwa njia ya mtandao mshitakiwa akiwa mahabusu Keko.
Na Mwandishi Wetu 

JAJI Mfawidhi wa Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Salma Maghimbi Juni 17 mwaka huu anatarajia kusikiliza maombi ya kuongeza muda wa kukata rufaa dhidi ya mfanyakazi wa benki Ibrahim Masahi, aliyeachiwa huru na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kinondoni.

Awali, ilidaiwa kuwa Masahi  Januari 11, 2023 akiwa eneo la Mbezi Msakuzi ndani ya Wilaya ya Ubungo mkoani Dar es Salaam alituhumiwa alimpiga Deogratus Minja kwa nyundo na kumsababishia kupata madhara makubwa ya mwili mwake.

Mahakama ya Kinondoni, baada ya kusikiliza kesi hiyo ya tuhuma za kujeruhi ilimuachia huru Masahi (mjibu maombi) kutokana na upande wa mashtaka kushindwa kuthibitisha shtaka bila kuacha shaka lolote.

Upande wa mashtaka kutokana na hukumu hiyo iliwasilisha kusudio la kukata rufaa kupinga hukumu hiyo iliyotolewa na Hakimu Mkazi Amos Rweikiza kwamba mshtakiwa katika ushahidi wake hakueleza jinsi alivyomtambua usiku wa tukio hilo.

Hata hivyo, upande wa mashtaka umedai kwamba katika kesi hiyo uliweza kuthibitisha shtaka kwa sababu shahidi wao alieleza jinsi alivyomtambua mshtakiwa Masahi kwa kutokana na mwanga wa taa uliyokuwepo eneo hilo la tukio.

Mjibu wa maombi (Masahi) kupitia wakili wake wamewasilisha majibu ya maombi yaliyowasilishwa mahakamani hapo na Jamhuri (kiapo kinzani).

Katika ushahidi wake, Minja alidai kuwa tarehe hiyo saa mbili na nusu usiku  alikuwa akipita nje ya geti la jirani yake Masahi, alimkuta kijana wa jirani huyo, baada ya kumuona alizungumza kwa kilugha kwa sauti kubwa ambae yeye hakuielewa. 

Amedai kuwa ghafla kijana alikwenda  mbele yake akamzuia asipite, geti likafunguliwa akatoka Masahi akimuhoji kwamba, yeye ni kama nani na amekwenda kumshtaki Serikali za Mitaa, ambapo hakumjibu kitu, kijana wa mjibu maombi akampiga ngumi.

"Aliinua shati lake juu akatoa nyundo akanipiga nayo kichwani baada ya kupata maumivu makali nilianza kukimbia huku nikipiga kelele za kuomba msaada," Amedai Minja.


MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam imesema Mei 6,2025 itatoa uamuzi dhidi ya mapingamizi yaliyotolewa na upande wa utetezi baada ya kusikiliza majibu yaliyotolewa na upande wa Jamhuri juu ya kesi ya kuchapisha taarifa za uongo mtandaoni inayomkabili Mwenyekiti wa Chadema Taifa Tundu Lissu kusikilizwa kwa njia ya mtandao.

Katika mapingamizi hayo, upande wa utetezi wanataka mteja wao (Tundu Lissu) afikishwe mahakamani hapo huku mshtakiwa mwenyewe akisisitiza kuwa kesi hiyo iendeshwe kwa uwazi ili kila mmoja apate kufatilia kinachoendelea.

Wakati mshtakiwa akitaka hivyo, upande wa Jamhuri ukiongozwa na Wakili wa Serikali Mwandamizi Job Mrema umesisitiza kuomba kesi hiyo isikilizwe kwa njia ya mtandao na kwamba iahirishwe kwa siku 30 ili kuwapa nafasi utetezi kujiandaa na pia kuwapa fursa ya kuwasiliana na mteja wao.

Kadhalika Upande wa Jamhuri umepinga hoja ya utetezi kwamba mteja wao alifanyiwa ukiukwaji wa kisheria wakati akihamishwa gereza kutoka Keko Kwenda Ukonga akisema kwamba hapakuwa na ukiukwaji wowote wa kisheria na haki yake haikuathiriwa popote. Amesema Magereza ilitekeleza utaratibu wao na hawakuwa na amri ya wapi anapaswa kupelekwa hivyo Magereza walikua sahihi.

Pia Jamhuri wameiomba mahakama isitoe amri yotote ya kumita Mkuu wa Magereza la Mkoa wa Dar es Salaam, Mkuu wa gereza la Ukonga na maafisa wa magereza ambao hawakutajwa majina yao kama utetezi walivyoomba, kwa sababu mahakama hii haina mamlaka ya kusikiliza hoja zinazohusu Jeshi la Magereza.

Katika majumuisho wa hoja zao, Upande wa Jamhuri umeiombao Mahakama izingatie ombi lao la kuahirisha kesi hiyo kwa siku 30 lakini pia Mahakama ipuuze hoja za Utetezi na ikubaliane na tafsiri ya Upande wa Serikali kwamba Mahakama mtandao ni Mahakama ya wazi.

Wakijibu hoja za upande wa Jamhuri, Mawakili wa utetezi wakiongozwa na Wakili Mpare Mpoki wameendelea kusimamia hoja zao kwamba mteja wao aletwe Mahakamani na si kusikiliza kesi hiyo kwa njia ya mtandao kwa kuwa inawatenga baadhi ya watu ambao hawana simu za kisasa yaani “Smartphone”

Akitoa hoja hiyo Wakili Mpoki amesema si wote watakua na uwezo wa kufuatilia kesi hiyo kwa njia ya mtandao lakini pia wapo wanaotegemea waandishi ambao nao wamezuiliwa kuingia mahakamani.

Utetezi wamejumuisha hoja zao kwa kuiomba Mahakama izingatie hoja zao na mteja wao afikishwe mahakamani na ipuuze hoja za Jamhuri.

Lissu alifikishwa kwa mara ya kwanza katika Mahakama ya Kisutu Aprili 10, 2025 akikabiliwa na kesi mbili moja ya uhaini na nyingine ya kuchapisha taarifa za uongo mtandaoni.

Kwa mujibu wa hati ya mahitaka, ilidaiwa mshtakiwa alitenda kosa hilo Aprili 3, 2025 jijini Dar es Salaam. Ilidaiwa kuwa Lissu akiwa ndani ya jiji la Dar es Salaam alitangeneza nia ya kushawishi au kuchochea umma ya kuweza kuzuia kufanyika kwa uchaguzi mkuu wa Tanzania kwa kusema maneno yafuatayo;

"Walisema msimamo huu unaashiria uasi, ni kweli kwa sababu tunasema tutazuia uchaguzi tutahamasisha uasi, hiyo ndio namna ya kupata mabadiliko....kwa hiyo tunaenda kukinukisha sanasana huu uchaguzi tutaenda kuvuruga kwelikweli, tunaenda kukinukisha vibaya sana.”


MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu imeelezwa kuwa, kesi dhidi ya wanandugu wawili na mwenzao mmoja wanaodaiwa kumuua kwa kukusudia ndugu yao Regina Chaula na kumtupa kwenye shimo la maji taka ndani ya nyumba yake bado haujakamilika

Ndugu hao ni Mkulima Mkazi wa Bagamoyo Fred Chaula (56), Dereva Bodaboda Mkazi wa Tegeta Bashiri Chaula (39) na mwenzao Denis Mhwaga (16) Mkazi wa Mafinga,Iringa.

Wakili wa serikali Tumaini Mafuru amedai hayo leo Machi 28,2025 wakati kesi hiyo ilipokuja kwa ajili ya kutajwa.

Kufuatia taarifa hiyo, Hakimu Mkazi Mkuu Rahim Mushi ameahirisha kesi hiyo hadi Aprili 3, 2025 washtakiwa wamerudishwa nyumbani.

Katika kesi hiyo washtakiwa kwa pamoja wanashtakiwa kwa kosa la mauaji ya kukusudia kinyume cha kifungu Cha 196 na 197 cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu kama ilivyorejewa mwaka 2019.

Inadaiwa, 18,2025 washtakiwa wakiwa eneo la Bahari Beach ndani ya Wilaya ya Kinondoni mkoani Dar es Salaam walimuua kwa makusudi Regina Chaula.

Awali,Fred na Bashiri walikamatwa na Jeshi la Polisi nchini kwa tuhuma za kumuua dada yao Regina wakati akiwa kwenye harakati za kufuatilia kesi zake za madai zilizopo katika Mahakama Kuu Divisheni ya Ardhi, Dar es Salaam.

Katika taarifa ya Jeshi hilo, ilidai kuwa Januari 18, 2025 askari walifika nyumbani kwa mama huyo na kubomoa shimo la maji take na kukuta mwili wa Regina, baada ya kutilia shaka shimo hilo ambalo lilikuwa limejengewa.
DAKTARI  kutoka Hospitali ya Polisi Kilwa Road, Denis Basyagile, ameieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kuwa kifo cha Robert Mushi kilisababishwa na kupoteza damu nyingi kutokana na majeraha mbalimbali mwilini.

Shahidi huyo aameeleza hayo wakati akitoa ushahidi wake katika kesi inayowakabili aliyekuwa Meya wa Manispaa ya Ubungo, Boniface Jacob, na mwenzake Godlisten Malisa, ambao wanakabiliwa na mashtaka ya kuchapisha taarifa za uongo mtandaoni dhidi ya kifo cha Mushi.

Akitoa ushahidi wake mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu Ushindi Swalo, Dkt. Basyagile ameeleza kuwa Aprili 23, 2024, alipokea agizo la kufanyia uchunguzi wa mwili wa marehemu Robert Mushi baada ya ndugu zake kufika hospitalini kwa ajili ya utambuzi.

Akiongozwa na wakili wa serikali Asiath Mzamiru kutoa ushahidi wake, Dkt. Basyagile ameeleza...

"Nilipofika mochwari, nilikuta askari aliyekuwa na amri kutoka mahakamani pamoja na ndugu wa marehemu, John Mushi na Magunda. Ndugu walithibitisha kuwa mwili huo ni wa Robert Mushi kwa kumtambua kwa sura."

Kwa mujibu wa daktari huyo, uchunguzi wa mwili ulifanyika saa 10 jioni, ambapo alibaini majeraha mengi usoni, mikononi, kifuani, tumboni na miguuni. "Sehemu za kifua na nyonga ya kulia zilikuwa zimebonyea, huku mbavu upande wa kulia zikiwa zimevunjika kuanzia mbavu ya tatu hadi ya tisa," ameeleza.

Aidha, Dkt. Basyagile amebainisha kuwa ini la marehemu lilipasuka, jambo lililosababisha damu nyingi kumwagika kwenye tumbo, huku nyonga yake ya kulia ikiwa imevunjika katika sehemu ya mfupa wa paja. "Chanzo cha kifo kilikuwa ni kupoteza damu nyingi kutokana na majeraha haya, ambayo mara nyingi hutokana na ajali za barabarani," ameeleza.

Baada ya uchunguzi huo, daktari huyo aliandika ripoti rasmi na kuikabidhi kwa askari aliyekuwa akisimamia uchunguzi wa tukio hilo lakini ripoti hiyo haikuwa na jina lake.

Hata hivyo mahakama imepokea ripoti hiyo kama sehemu ya ushahidi katika kesi hiyo.

Baada ya kumaliza kutoa ushahidi wake, wakili wa utetezi, Peter Kibatala, alimtaka shahidi kueleza iwapo aliwahoji askari au ndugu wa marehemu kuhusu kilichosababisha kifo chake. Dkt. Basyagile alijibu kuwa hakufanya hivyo.

Aidha, wakili huyo alihoji kuhusu uwepo wa mgongano wa maslahi, ikizingatiwa kuwa hospitali ya Polisi Kilwa Road iko chini ya Jeshi la Polisi, ambalo ndilo linahusiana na kesi hiyo. Hata hivyo, daktari huyo alieleza kuwa hajui kama kilichopelekea uchunguzi ni tuhuma dhidi ya Jeshi la Polisi.

Mahakama ilifahamishwa kuwa mwili wa marehemu ulikuwa umekaa hospitalini hapo kwa siku 12 kabla ya kufanyiwa uchunguzi. Hata hivyo, daktari huyo hakueleza ni kwa nini ripoti yake haikuwa na majina ya mashahidi waliokuwepo wakati wa uchunguzi huo.

Kesi hiyo inamkabili aliyekuwa Meya wa Manispaa ya Ubungo, Boniface Jacob, na mwenzake Denis Basyagile, wakidaiwa kuchapisha taarifa za uongo mtandaoni. Kesi inaendelea kusikilizwa mahakamani.

Jacob na mwenzake wanakabiliwa na mashitaka matatu likiwemo la kusambaza taarifa za uongo kwa lengo la kupotosha umma.

Wanadaiwa, Aprili 22 mwaka huu ndani ya mkoa na jiji la Dar es Salaam, Jacob kwa lengo la kupotosha umma , alisambaza taarifa za uongo lkupitia mfumo wa kompyuta wenye jina la Boniface Jacob @ExmayorUbungo wenye kichwa kilichosomeka 'wenye leseni ya kuua wameua Tena'.

Taarifa hiyo ilieleza 'kijana wetu Rajabu Mlanga Mushi maarufu kama Babu G, amekutwa Hospitali ya Kilwa Road akiwa ameuwawa. Imagine tumetoa taarifa Jeshi la polisi la kupotelewa kwa kijana wetu , cha ajabu Jeshi la polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam likawa linatusaidia kumtafuta pia'

'Kila siku jeshi la polisi linasema halijapata taarifa wala fununu zozote za kijana wetu na kwamba tuwe wavumilivu wanapambana kuendelea kumtafuta .Jana machale yakawacheza ndugu wa kijana baada ya msiri mmoja kuwatonya ndugu 'nendeni hospitali ya polisi Kilwa road mkachungulie vyumba vya kuhifadhia maiti'.

'Ndugu walivyokwenda huko hospitali ya polisi Kilwa road wakamkuta kijana wao akiwa ameuwawa, wahusika wa hospitali wanadai maiti ililetwa tangu tarehe 10 Aprili mwaka 2024, na na askari wa Jeshi la polisi'.

'Maiti ina siku 12 katika hospitali ya polisi Kilwa road bila jeshi la polisi kujua ipo hapo?..., polisi aliyepeleka maiti ni wa nchi gani?, walipoombwa kujua ni askari wa kituo gani na majina yao ni yapi ,wahusika wa hospitali hiyo ya polisi wanadai hawajui na wanaomba wasitajwe...'.

'Wacha wanyonge tukazike maiti zetu, sitamani hata kuona ndugu wakiomba uchunguzi dhidi ya maiti yao kwasababu hata mtoto mdogo anajua hapo Muuaji ni nani'.

'Pili tunajua ile mbinu ya 'TAPE', ile kufunga mtu miguu , kufunga mikono kisha kupigwa tape ya mdomo na puano hadi kifo baada ya ile mbinu ya kupeleka msituni ,porini na kupigwa risasi kujulikana. Dar es Salaam ina mtu mmoja katili sana'.

Jacob anadaiwa kusambaza taarifa ya uongo kupitia mfumo wa komoyuta wenye jina la X , kwa jina la Boniface Jacob @ExMayorUbungo wenye kichwa kisomekacho ' Mauaji Arusha'.

'Mwananchi mwenzetu na aliyekuwa dereva wa magari ya watalii Omary Msamo ameuwawa na skari wa Jeshi la polisi wilaya ya Karatu Mkoa wa Arusha'.

'Omary Msamo ameuwawa baada ya kusimamishwa na kushushiwa kipigo kizito kilichopelekea kutoa uhai wake na polisi wa usalama barabarani baada ya kutuhumiwa kuendesha gari akiwa ametumia kilevi'.

'Kwamba, jeshi la polisi linatumia kila jitihada kuzuia vyombo vya habari kuripoti tukio hili kama nia ya kuficha na kuwanusuru askari wake dhidi ya mkono wa sheria' .

Mshtakiwa Malisa pekee anadaiwa kuwa kwamba, kwalengo la kupotosha umma , alisambaza taarifa za uongo kupitia mfumo wa kompyuta , kwenye akaunti ya Instagram ya jina la Malisa_gj.

Taarifa hiyo ilisomeka kwamba 'Aprili 13 Meya mstaafu wa Manispaa ya Ubungo @exmayor_bonifacejacob alitoa taarifa ya kupotelewa na ndugu yake Bw. Robert Mushi maarufu kama Babu G, ambaye alipotea mapema mwezi Aprili 2024'.

'Inadaiwa alikamatwa na watu waliojitambulisha kuwa polisi maeneo ya Kariakoo na baada ya hapo hakuonekana tena'.

'Leo wakaambiwa nendeni hospitali ya polisi Kilwa road ndugu yenu amefichwa monchwari pale

wakaenda. Lahaula!, wakamkuta Robert akiwa katika jokofu la baridi, hakuwa Robert tena bali mwili wake ukiwa na majeraha ya kipigo' .

'Ni mauaji ya kikatili, Maskiki Robert hajawahi kuwa na ugomvi na mtu , kwanini atendewe haya?'.
Kesi hiyo Inaendelea kesho Machi 18, 2025


RAIA mmoja wa Ghana na watanzania watatu wamefikishwa katika mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na kesi ua uhujumu uchumi yenye mashtaka manne likiwemo la utakatishaji wa zaidi ya Sh. Bilioni mbili.

Katika hati ya mashtaka iliyosomwa mahakamani hapo na wakili wa serikali Tumaini Mafuru imewataja washtakiwa hao kuwa ni Valentine Kof (45) raia wa Ghana anayeishi Mikocheni, Patrick Tarimo(34) mkazi wa Kibaha, Aisha Kagashe (40) anayeishi SInza na Idan Msuya (46), mkazi wa Mikocheni.

Washtakiwa hao ambao wamesomewa mashtaka yao mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi Jofrey Mhini, katika shtaka la kwanza wanadaiwa kutenda kosa la kuongoza genge la uhalifu kati ya Septemba Mosi 2021 na Oktoba

25, 2021 huko katika maeneo ya Arusha na Dar Es Salaam nchini Tanzania, Ghana, Ivory Coast, Uganda, Zambia, Senegal, Cameroon, France Mali na Burkina Faso

Inadaiwa katika kipindi hicho washtakiwa wakiwa pamoja na watu wengine ambao hawapo mahakamani waliongoza genge la uhalifu kwa kuingilia mfumo wa kompyuta wa benki ya African Banking Corporation Tanzania Ltd (Bank ABC) kinyume cha sheria kwa lengo la kutenda kosa la wizi na hivyo waliiba Sh. 2,095,170,000

katika shtaka la pili imedaiwa katika kipindi hicho hicho washtakiwa kwa pamoja wakiwa na watu wengine ambao hawapo mahakamani kwa makusudi walisababisha mfumo wa ABC benki kuingiliwa na Akaunti ya Visa ya malipo ya awali (Pre-Paid Visa) ipokee malipo ya Sh. 3,543,555,243'37

Wakili Mafuru ameendelea kudai kuwa katika tarehe hizo na mhali hapo hapo washtakiwa waliiba Sh. 2,095,170,000 kwa njia ya kuzitoa kupitia mfumo wa Kadi ya Visa ya malipo ya awali (Pre-Paid Visa) kutoka kwenye utambulisho wa benki namba (BIN) 486054 mali Benki hiyo

Washtakiwa pia wanakabiliwa na shtka la utakatishaji ambapo wanadaiwa kujipatia kiasi che fedha hizo zaidi ya Sh. Bilioni mbili mali ya benki hiyo wakati wakijua kuwa fedha hizo ni zao la kosa tangulizi la wizi.

Hata hivyo washtakiwa hawakuruhusiwa kujibu kitu chochote mahakamani hapo kuwa mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza kesi za uhujumu uchumi.

kwa mujibu wa upande wa mashtaka upelelezi katika kesi hiyo bado haujakamilika na washtakiwa wamerudishwa rumande hadi Machi 26,2025 kesi hiyo Itakapokuja kwa ajili ya kutajwa
Jengo la Mahakama Kuu ya Tanzania, Division ya Ardhi

MAHAKAMA Kuu Divisheni ya Ardhi imefanikiwa kutatua mgogoro wa zaidi ya miaka 20 uliohusisha umiliki wa nyumba, ambayo aliyekuwa Mtaalamu wa Shirika la Maendeleo la Taifa, Regina Ishemwabura, aliinunua kutoka Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) mwaka 1973.

Jaji Elinaza Luvanda ametoa uamuzi huo hivi karibuni dhidi ya Nasor Hamis, John Mwanga na Fisha Mashoo,walalamikiwa,  baada ya kumtangaza Regina, mlalamikaji, kuwa ndiye mmiliki halali wa nyumba hiyo ya makazi iliyopo Kiwanja namba 705 Block ‘F’ iliyotambulika awali kuwa ni nyumba iliyopo Kiwanja namba 94A Drive Inn Cinema, Msasani.

Tayari Mahakama imemwamuru Dalali, Joshua Mwaituka, anayefanya shughuli hizo kupitia Fosters Companies Limited, kuwafukuza wadaiwa hao na kuwaondoka mara moja katika nyumba hiyo, iliyopo kando ya Barabara ya Bagamoyo.

Aidha, Mahakama imemuagiza Dalali wa Mahakama huyo kuondoa mabadiliko yote yaliyofanywa na wadaiwa bila kuathiri nyumba na kuwafukuza kwa kuvunja nyumba tajwa ili kumwezesha mmiliki halali,  Regina kuingia.

‘Unaamuriwa  pia kurudisha hati hii siku au kabla ya tarehe 10 Aprili, 2025, ikionyesha namna amri hii imetekelezwa au kushindwa kutekelezwa,’ inasomeka sehemu ya amri hiyo  iliyosainiwa Machi 10, 2025 na Naibu Msajili, Mwajuma Lukindo.

Katika hukumu yake, Jaji Luvanda amepitia ushahidi uliotolewa na mashahidi watano wa upande wa Mlalamikaji na kujiridhisha kuwa Regina ndiye mmiliki halali wa nyumba hiyo iliyopo Kiwanja namba 705 kitalu ‘F’ ambayo awali ilitambulika kuwa ni nyumba iliyopo Kiwanja namba 94A Drive Inn Cinema Msasani kando ya Barabara ya Old Bagamoyo.

Miongoni mwa ushahidi uliotolewa ni pamoja na ule wa Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni, kumthibitishia mlalamikaji kuwa ni mmiliki halali wa nyumba hiyo na ushahidi wa Benki ya Rasilimali Tanzania, ambapo alipata mkopo wa kununua nyumba na ripoti ya uchunguzi wa polisi juu ya madai ya kughushi, ambayo pia ilionesha kuwa hakuwa na hatia.

'Kwa maoni yangu, kesi ya Mlalamishi iliwasilishwa vizuri na ushahidi uliotolewa ulithibitisha kuwa ana hati miliki nzuri juu ya mali hiyo. Kwa ushahidi mwingi na ripoti hiyo, haishangazi ilikuwa ndiyo sababu ya Nasor Hamis alikwepa kujitetea,' Jaji Luvanda alisema.

Wakati wa kusikilizwa kwa shauri hilo, John Mwanga na Fisha Mashoo hawakufika mahakamani wala kuwasilisha hati ya utetezi kwa maandishi, hivyo shauri hilo liliendelea bila pande zote mbili kusikilizwa.

Vile vile, maelezo ya maandishi ya utetezi ya Nasor Hamis yalikataliwa baada ya kukaidi kuwasilisha maelezo ya mashahidi kama ilivyoamriwa Machi 5, 2024 na kukataa kuhudhuria tarehe na wakati ambao walipaswa kujitetea.

Mlalamikaji anadaiwa kununua nyumba hiyo kutoka kwa Shirika la Nyumba la Taifa chini ya mpango wa ununuzi wa upangaji uliendeshwa na Benki ya Nyumba Tanzania (THB).

Ilidaiwa na Mdai kuwa baada ya kununua, alikaa katika nyumba kuanzia 1973 hadi 1976 alipohamia Nairobi kuungana na mumewe, na kuacha nyumba chini ya ulinzi wa rafiki yake, Pucharis Kashaija.

Baadaye Kashaija aliihama nyumba hiyo baada ya watu fulani wanaodaiwa kuinunua. Ilikuwa ni ushahidi wa Mdai kuwa aliporudi kwenye nyumba hiyo alimkuta Karibu Ismael anayedaiwa kuingizwa humo na mjomba wake, Nasor Hamis.

Mlalamikaji anadaiwa kumfukuza Karibu Ismael kupitia amri iliyotolewa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam. Alidai kuwa nyumba ilikabidhiwa kwake mnamo 1997 ambapo aliipangisha kwa mtu mwingine.

Kwa mujibu wa mlalamikaji, mwaka 2006 aliporudi alimkuta mpangaji wake ameondoka na John Mwanga alivamia nyumba hiyo. Alidai kuwa mwaka 2007 alipokuwa anachakata hati iligundulika kuwa mali hiyo namba 94A ilipimwa upya na kupewa jina jipya la Plot No. 705 Block A.

Mlalamikaji alidai kuwa shauri hilo lilichunguzwa polisi na Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai, ambapo ilibainika kuwa hatimiliki ya Nasor Hamis ilitoka kwa Fisha Mashoo aliyemuuzia John Mwanga, ambaye ndani ya mwezi mmoja aliiuza kwa Nasor Hamis.

Na Farida Mangube,Morogoro

MAHAKAMA Kuu ya Tanzania Kanda ya Morogoro imetupilia mbali shauri la madai namba 5 la mwaka 2023, kesi iliyofunguliwa na Nkumbi Marashi Holela na wenzake 47 chini ya Wakili wao Yudathade Paul dhidi ya Mussa Ginawele na Anna Ballali walio kuwa wakiwakilishwa na Wakili Rabin Mafuru kuhusu umiliki wa shamba namba 512 lenye hati ya miliki wa aliyekuwa Gavana wa Benk kuu ya Tanzania Daud Balali.

Kesi hiyo iliyokuwa ikisikilizwa na Jaji Muruma ilitolewa hukumu na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Morogoro Suzan Kihawa Februari 21 mwaka huu baada ya Mahakama kukamilisha taratibu zote ikiwemo kusikiliza ushahidi uliowasilishwa na pande zote mbili.

Ambapo amesema upande wa walalamikaji wameshindwa kuithibitishia Mahakama madai saba waliyowasilisha mahakamani hapo.

Madai saba yaliyowasilishwa mahakamani hapo ni pamoja na eneo lenye mgogoro litamkwe kuwa linamilikiwa na walalamikaji, kitendo cha wadaiwa kuripoti polisi na kufanya alasemiti kitamkwe kwamba kimewanyima haki ya umiliki.

Madai namba mbili hamiliki ardhi katika eneo lenye mgogoro , malipo ya fidia kiasi cha Sh.million sita kutokana na usumbufu wa kisaikolojia na amri ya gharama ya uendeshaji wa kesi pamoja na riba ya asilimia 12 ya kiasi kilichombwa kutoka siku ya hukumu mpaka kitakapolipwa .

Baada ya kusikiliza pande zote mbili imeamuriwa upande wa walalamikaji umeshindwa kuithibitishia Mahakama hiyo , hivyo kutoa haki kwa Christopher Ginawele na Anna Ballali.

Wakati nje ya Mahakama ,Wakili wa upande wa wadaiwa Rabin Mafuru amesema wameridhishwa na hukumu hiyo ambayo ni udhihirisho kuwa Mahakama za Tanzania zinaendelea kusimamia haki,ingawa kuna wakati inachelewa lakini mwisho inapatikana

Ameongeza hata kabla ya kesi hiyo kulikuwa na kesi kadhaa tangu mwaka 2017 kutoka kwa watu hao hao lakini kesi hizo hazikufikia hatua za kusikilizwa kutokana na upungufu wa kisheria.

Pia amesema kuwa haki inapotendeka inaongeza heshima na funzo kwa wengine wenye tatia kama hizo huku akikiri kuwepo uhitaji mkubwa wa maboresho katika sheria hususani za umiliki ardhi na namna ya kushughulikia migogoro ya ardhi kwani bado kuna mianya mingi inawapa nguvu wavamizi wa ardhi dhidi ya wamiliki halali wenye nyaraka.

“Kulinganisha mtu mwenye hati na asiye na hati sioni kama tunamtendea haki mmiliki wa hati na serikali iliyotoa hiyo hati, naelewa msingi wa hatua za kisheria katika kutatua migogoro, hizi sheria inabidi tuzifanye ziendane na mazingira yetu...

"Kwani wavamamizi wanatumia hii mianya kupeleka madhara na hasara kwa wamiliki halali wenye nyaraka, kama wakili ni sehemu ya mahakama ,natoa maoni kama mdau wa haki,Bunge ndio lenye wajibu wa kufanya marekebisho ya sheria,kuona kama kuna haja ya kuendelea na taratibu za kisheria tulizorithi kwa Wakoloni,"amesema Wakili Rabin Rutabhu Mafuru.

Kwa upande wake Mwakilishi wa upande wa washitaki Nkumbi Holela akizungumza kwa njia ya simu amesema wamepokea hukumu hiyo na bado wapo katika majadiliano kama watakata rufaa kuendelea na shauri hilo katika ngazi nyingine ya Mahakama au laa.

"Tumepokea hukumu kwa vile Mahakama ndio yenye uamuzi wa mwisho wa kutoa haki, tumeipokea ila kwa upande wetu bado kidogo tunamjadala kuhusu kukata rufaa."

Kesi hiyo Namba 5 ya mwaka 2023 ilifunguliwa na Wakulima 48 wakazi wa kiongozwa na Nkumbi Marashi Holela dhidi ya wadaiwa wawili Mussa Ginawele (Msimamizi wa Shamba) na Anna Muganda Ballalli ambaye ni mjane wa marehemu Daudi Ballali aliyekuwa Gavana ya BoT.

Kesi hiyo ilifunguliwa Mahakama Kuu ya Tanzania kanda ya Morogoro na kusikilizwa na mbele ya Jaji Mruma.


 

Na Karama Kenyunko Michuzi Tv

RAIA nane wa Pakistan wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi yenye mashtaka ya kusafirisha zaidi ya kilo 400 za dawa za kulevya.

Katika  hati ya mashtaka iliyosomwa mahakamani hapo na wakili wa serikali Titus Aron imewataja washtakiwa hao kuwa ni Mohamed Habifu (50), Mashaal Yusuph (46), Imtiaz Ahmed (45), Tayab Pettilwam (50),Immambakish Kudhabakish (55), Chand Mashaal (29), Akram Hassan (39) na Shehzal Hussein (45)

Imedaiwa mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Beda Nyaki kuwa, Novemba 25, 2024 huko katika eneo la Navy Kigamboni jijini Dar es salaam washtakiwa wote walikutwa wakisafirisha  kilo 22.53 za dawa za kulevya aina ya heroine na kilo 424.77 za dawa za kulevya aina ya Methamphetamine.

Hata hivyo washtakiwa baada ya kusomewa mashtaka yao hawakuruhusiwa kujibu kitu chohote mahakamani hapo kwa kuwa mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza kesi za uhujumu uchumi ambazo kwa kawaida husikilizwa Mahakama Kuu ama kwa kupewa kibali kutoka kwa DPP

Kwa mujibu wa upande wa mashtaka upepelezi katika kesi hiyo bado haujakamilika na kesi imeahirishwa hadi Januari 22, 2024 kwa ajali ya kuja kutajwa. Washtakiwa wote wamerudishwa rumande.






 

 

Na Jane Edward,Arusha .


Waziri Mkuu amewakumbusha Majaji na Mahakimu wa Ukanda wa Afrika Mashariki kuendelea kutumia matumizi ya teknolojia kwani  ni muhimu kuzingatiwa kwa kufikia utoaji wa haki wenye ufanisi.

Akizungumza wakati wa kufungua Mkutano Mkuu wa 21 wa Chama cha Mahakimu na Majaji wa Afrika Mashariki (EAMJA) kwa niaba ya Rais Dkt Samia Suluhu Hassan Mkoani Arusha.

Amesema kuwa, Serikali ya Tanzania inaiheshimu Mahakama na inaunga mkono kikamilifu juhudi zake za kuwezesha mfumo wa utoaji haki kuwa wa kisasa.

Hata hivyo Majaliwa amesema kuwa ,mifumo imara ya Mahakama katika utoaji wa haki ni muhimu na ina mchango mkubwa katika ukuaji wa uchumi hivyo ni jambo la muhimu ukaendelea kuzingatiwa.

“Mfumo ulioimarishwa wa utoaji wa haki ndani ya Mahakama ni muhimu kwa ujumuishaji wa kina wa kikanda na ukuaji wa uchumi, nikiwa kama mmoja wa viongozi katika ukanda huu, ninathamini sana mikusanyiko ya kikanda kama hii, ambayo huwaleta pamoja Mahakimu na Majaji wa Afrika Mashariki kushughulikia masuala muhimu ya kitaifa na kikanda yanayolenga kutoa haki na hatimaye kukuza uchumi wa ukanda huu,” amesema Waziri Mkuu. 


Aidha, amepongeza Viongozi wa Chama cha Mahakimu na Majaji wa Afrika kwa kuchagua Kaulimbiu isemayo, ‘Uboreshaji wa mifumo ya utoaji haki kwa ajili ya kuimarisha utengamano na Ukuzaji Uchumi katika Ukanda wa Afrika Mashariki’ kwa kuwa inahimiza ustawi wa haki kwa wananchi ambao unaleta amani na utulivu na hatimaye kukuza uchumi.

Amesema kusanyiko hilo litatoa fursa ya kuchanganua changamoto zinazoukabili ukanda huo katika kutoa haki na kuandaa mikakati ya kukabiliana nazo na kwamba mwavuli wa EAMJA unawawezesha kushirikiana katika kuhakikisha haki yenye ufanisi na shirikishi kwa wananchi wa ukanda huo.

Ameongeza kuwa, nchini Tanzania, chini ya uongozi wa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kumefanyika uamuzi muhimu ya kisera ya kijamii na kiuchumi ambayo yanajenga muelekeo wa maendeleo, yenye lengo la kuboresha ustawi na ustawi wa watu wa Tanzania. 

“Sera hizi ni pamoja na, miongoni mwa nyingine, kuzingatia kuimarisha uwezo wa kitaasisi ndani ya mfumo wa utoaji haki kwa njia ya kisasa. Lengo ni kukuza haki za kimsingi za mtu binafsi, kuimarisha mchango wa Mahakama katika mazingira mazuri ya uwekezaji, na kuboresha utumiaji wa teknolojia za kisasa ili kusaidia Mahakama inayozingatia raia, inayohakikisha utoaji wa haki kwa ufanisi, uwazi na kwa wakati,” ameeleza Mhe. Majaliwa.


“Serikali yetu inaamini kuwa upatikanaji wa haki ni nguzo ya msingi inayosukuma mbele malengo ya Dira ya Maendeleo ya Tanzania 2025 na lengo la Maendeleo Endelevu namba 16, ambalo linajitolea kukuza jamii zenye amani na ushirikishi kwa maendeleo endelevu, kuhakikisha upatikanaji wa haki kwa wote, na kujenga taasisi zenye ufanisi, zinazowajibika katika ngazi zote," amesisitiza Waziri Mkuu.


Naye Waziri wa Katiba na Sheria, Prof. Palamagamba Kabudi amesema, Majaji na Mahakimu na watu muhimu wenye kuchangia amani na utulivu wa watu na nchi kwa ujumla.

“Mtu yeyote anahitaji kupata haki yake, sehemu anayokimbilia ni Mahakama kutafuta haki, hivyo wananchi wanawaamini ninyi na wana imani kuwa wanapokuja kwenu wanajua watapata haki zao, hivyo ni muhimu kuilinda imani hii kwa kutekeleza kile ambacho mmekasimiwa kwa mujibu wa sheria,” amesema Prof. Kabudi.


Naye Jaji Mkuu wa jamhuri ya muungano wa Tanzania Prof. Ibrahim Juma amesema kuwa tunapoimarisha utoaji wa mfumo wa haki, na mamlaka zetu zikitoa rasilimali za kutosha ili kuimarisha haki na taasisi za mahakama, taratibu na taratibu, mfumo wa haki utachangia ukuaji wa uchumi wa taifa na ushirikiano wa kikanda wa Afrika Mashariki. 


Amesema kuwa ,mkutano huo wa Mahakimu na Majaji wa Afrika Mashariki na Mkutano wa Mwaka unahusu "Kaulimbiu ya Kuimarisha Mfumo wa Utoaji Haki kwa Mtangamano wa Kikanda na Ukuaji wa Uchumi."

"Mada hii inazingatia imani yetu ya pamoja kwamba sekta za kitaifa za sheria na haki ni muhimu ili kuanzisha hatua kwa hatua Umoja wa Forodha, Soko la Pamoja, Muungano wa Fedha, na hatimaye, shirikisho la kisiasa. Juhudi za Viongozi wa Afrika Mashariki za kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi lazima ziende sambamba na kuwezesha mahakama za kitaifa zenye ufanisi, zenye ufanisi na za haki.


Aidha Jaji Mkuu Prof .Juma amesema kuwa, mada ya mkutano wetu inatukumbusha, tunapoimarisha utoaji wa mfumo wa haki, na mamlaka zetu zikitoa rasilimali za kutosha ili kuimarisha haki na taasisi za mahakama, taratibu na taratibu, mfumo wa haki utachangia ukuaji wa uchumi wa taifa na ushirikiano wa kikanda wa Afrika Mashariki. .


Amesema kuwa ,Kongamano na mikutano ya kila mwaka huwapa fursa nyingi za kujifunza na kubadilishana. ambapo kila moja ya mamlaka yetu imeanza vipengele mbalimbali vya mageuzi ya mahakama. Tuna uzoefu wa kushiriki kuhusu mageuzi katika mifumo yetu ya haki ya jinai na jinsi ambavyo tumekumbatia teknolojia inayobadilika haraka ili kuhakikisha wananchi wanapata haki kwa ufanisi na upesi bila kuchelewa.

 



MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu imemuachilia huru kwa dhamana aliyekuwa Meya wa Kinondoni na Ubongo jijini Dar es Salaam, Boniface Jacob 'Boni Yai' baada ya kutupilia mbali pingamizi la upande wa Jamuhuri la kuzuia dhamana dhidi yake.


Uamuzi huo umetolewa leo Oktoba 7,2024 na
Hakimu Mkazi Mfawidhi Franco Kiswaga wa mahakama hiyo, wakati kesi hiyo ilipokuja kwa ajili ya uamuzi wa kama mshtakiwa apatiwe dhamana au la.

Akisoma uamuzi huo Hakimu Kiswaga amesema kuwa kiapo cha Mkuu wa upelelezi Mkoa (RCO) wa Mkoa wa Polisi Kinondoni Davis Msangi hakina maelezo ya kutosha kuzuia mshtakiwa asipate dhamana hiyo.

Amesemaa, maelezo yaliyotolewa hayana maelezo ya ziada ya kwanini mahakama isitoe dhamana. Iwapo mjibu maombi ametoa maelezo juu ya usalama wake nilitegemea muombaji (Jamhuri) ataleta uthibitisho juu ya maelezo ya Mjibu maombi.

Pamoja na kwamba upande wa majibu maombi haujaleta kiapo kinzani lakini kiapo cha muombaji hakitoshi mahakama kumnyima dhamana mtuhumiwa ukizingatia hii ni haki ya kikatiba .

Mahakama hii haikubali maombi ya Jamhuri hivyo basi mjibu maombi amepewa dhamana kwa masharti ya kuleta wadhamini wa wawili wenye barua za serikali ya mtaa ambao kila mmoja atasaini bondi ya Sh. Milioni saba na pia haruhusiwi kusafiri nje ya nchi bila kibali cha mahakama.

Jackob amepatadhamana baada ya kusota rumande kwa takribani siku 19 ambapo alifikishwa mahakamani kwa mara ya Septemba 19,2024 akikabiliwa na tuhuma za kuchapisha taarifa za uongo kupitia mtando wake wa X zamani Twitter.

Katika kesi hiyo Boni Yai anakabiliwa na mashtaka mawili, ya kuchapisha taarifa za uwongo katika mfumo wa kompyuta katika akaunti ya X yenye jina la Boniface Jacob @Ex MayorUbungo kwa nia ya kupotosha umma kinyume na kifungu cha 16 cha Sheria ya Makosa ya Kimtandano namba 14 ya mwaka 2015.

Katika shtaka la kwanza Wakili Manja alidai kuwa , Septemba 12 2024 jijini Dar alichapisha taarifa za uwongo zikimhusisha Mkuu wa Upelelezi wa Kanda (ZCO) ya Dar Es Salaam, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP).

" Mafwele anatuhumiwa na familia nyingi kama mtu ambaye ameshiriki mauaji kwa moja katika kuwapoteza ndugu wa baadhi ya familia zao, kupotea kwa mfanyabiashara Mussa Mziba, kupotea kwa Deo Mugasa, kupotea kwa Adinani Hussein Mbezi, kupotea kwa vijana watano wa Aggrey" .

Katika shtaka la pilia Wakili Manja alidai kuwa Boni Yai alitenda kosa hilo Septemba 14, 2024 jijini Dar es Salaam akidaiwa kuchapisha taarifa za uwongo kuwa zinazowahusisha Wakuu wa Upelelezi wa mikoa na utekaji na mauaji ya watu na kutupa miili yao.

Ujumbe huo unasomeka "mkawasifia Ma-RCO (Wakuu wa Upelelezi Mikoa) wanaozuia uhalifu kwa kutenda uhalifu ..., bali Ma-RCO waliokuwa kuteka, kukamata, kupiga watuhumiwa risasi, kuwafunga tape, kuwafunga mifuko ya nailoni usoni na kisha kutupa miili ya watuhumiwa ndio wanaijua kazi ya upolisi,"
 



Na Karama Kenyunko
MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kinondoni, inatarajia kusikiliza mashahidi 40 na kupokea vielelezo 480 katika kesi ya uhujumu uchumi inayowakabili wakazi wanne wa Dar es Salaam, wanaodaiwa kuisababishia Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) hasara ya Sh milioni 971.7

Washtakiwa hao Frank Kagale, fundi wa mashine za kielektroniki za EFD, Awadhi Mhavile (39) Ally Msesya maarufu kama Ally Yanga (37) Mkazi wa Pugu na Salma Ndauka (38) Mkazi wa Sinza na Msimamizi wa Gereji wanakabiliwa Na jumla ya mashtaka 574 yakiwemo ya kughushi.

Wakili wa Serikali Tumpale Lawrence akisaidiana na Wakili wa Serikali Mwandamizi, Emmanuel Medalakini na Wakili wa Serikali, Auni Chilamula amedai mbele ya Hakimu Kupa kuwa shauri hilo leo Septemba 12,2024 lilikuja kwa ajili ya kusikilizwa hoja za awali kufuatia upelelezi kukamilika.

Akisoma hoja hizo, Wakili Tumpale alidai mbele ya Hakimu Mfawidhi Is-haq Kuppa kuwa, Machi, 2023, TRA ilipokea taarifa kutoka kwa msiri kuwa kuna risiti za kielektroniki zilizotolewa kutoka kwenye mashine zilizopotea au kuibwa kutoka kwa wamiliki halali na zinasambazwa isivyo halali.

Anadai kuwa kutokana na taarifa hiyo uchunguzi ulianza kwa kushirikiana na maafisa wa Jeshi la Polisi na ndipo Julai 7, 2023 mtu aitwae Meshack Athanas dereva wa pikipiki maarufu kama bodaboda alikutwa na risiti za kielektroniki saba za Sh 128,500,000.

Anadai kati ya risiti hizo nne zilikuwa zimetolewa kutoka kwenye mashine ya kieletroniki mali ya Africa Harmony and Trade Ltd yenye namba 03TZ843040152 aliyesajiliwa kwa namba ya mlipakodi 159265420.

"Risiti mbili zilitolewa kutoka kwenye mashine ya kieletroniki mali ya Tabisco Entreprises ltd yenye namba 03TZ442007272 na namba ya mlipa kodi ni 100219557 na risiti moja iliyotolewa kutoka kwenye mashine ya kieletroniki mali ya Eco Consumer Products ltd yenye namba 03TZ442021550. Katika maelezo ya Athanas alieleza kupewa risiti hizo na Ally Omary Msesya ambae ni mtuhumiwa namba tatu," alidai Tumpale.

Katika tarehe hiyo hiyo, Athanas aliwaongoza wapelelezi katika ukamataji wa mshtakiwa Msesya na Julai 8, 2023 Athanas aliwaongoza wapelelezi kumkamata mshitakiwa Mhavile.

Anadai baada ya kukamatwa mshtakiwa Mhavile alikutwa na risiti za kieletroniki 11 zisizosahihi au za uongo zenye thamani ya Sh 133, 000,000 zikiwa zimetolewa kutoka kwenye mashine ya kieletroniki yenye namba 03TZ843040152 mali ya Africa Harmony Industry and Trade Ltd na mashine nyingine za kieletroniki 13 kampuni ya INCOTEXT zikisadikika kuwa za wizi au zimepatikana kinyume cha sheria na mashine hizo zilihodhiwa.

Pia anadai katika kumhoji mshtakiwa Mhavile alimtaja mshtakiwa Kagale kuwa ndiye mwenye mashine iliyotumika kutoa risiti hizo zisizo sahihi alizokutwa nazo.

"Kutokana na maelezo ya Mhavile juhudi za kumtafuta Kagale zilianza na Julai 19, 2023 wapelelezi walipokea taarifa kutoka kwa msiri kuwa Kagale ana rafiki wa kike aitwae Salma Ndauka ambae ni mshtakiwa namba nne," aliendelea kudai.

Julai 19, 2023 alikamatwa na katika upekuzi alikutwa na mashine 10 za kieletroniki aina ya INCOTEX ambapo mashine nane ndizo zilitambulika namba zake na mashine mbili hazikutambulika kwani zilifutika na kwamba mashine hizo zilihodhiwa.

Vilevile alidai, wakati wa kumhoji mshitakiwa Ndauka alimtaja pia Kagale kuwa ndiye mwenye mashine hizo.

Wakili Tumpale alidai kuwa Januari 16, mwaka huu Kagel3 alikamatwa na katika mahojiano alikiri kuwa mashine za kieletroniki alizokutwa nazo mshtakiwa Ndauka ni za kwake na alikiri kutumia mashine hizo kutoa risiti mbalimbali za kieletroniki zisizosahihi.

Kwa mujibu wa Tumpale, uchunguzi ulibaini kuwa mashine yenye yenye namba 03TZ443024331 mali ya Kampuni ya Oceanic Cachet katika kipindi cha kati ya Aprili, 2023 na Julai, 2023 ilitumika kutoa risiti ya za uongo au zisizo sahihi za Sh 1,932,096,214.28 na kutokana na kiasi hicho jumla ya kiasi cha Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) ya Sh 294,726,540.37 hakikuwasilishwa Mamlaka ya Mapato Tanzania.

Alidai mashine yenye namba 03TZ442007272 mali ya Tabisco Enterprises ltd katika kipindi cha kati ya Aprili, 2023 na Juni, 2023 ilitumika kutoa risiti ya za uongo au zisizo sahihi za Sh 2,375,310,754.61 na kwamba kiasi cha Sh 373,537,333.9 kama VAT hakikuwasilishwa TRA.

Pia alidai mashine yenye namba 03TZ843040152 mali ya Africa Harmony lndusry and Trade ltd katika kipindi cha kati ya Mei, 2023 na Juni, 2023 ilitumika kutoa risiti ya za uongo au zisizo sahihi zenye jumla ya Sh 1,929240,063.00 na Sh 303,713,897.37 kama VAT hakikuwasilishwa TRA.

Anadai kutokana na hali hiyo, waliisababishia hasara ya Sh 971,977,772.32 na kwamba walipotosha mfumo na Kamishna Mkuu wa kwa kuonesha kuwa Kampuni ya Oceanic Cachet imefanya mauzo ya Sh 1,932,096,214.28, Kampuni ya Tabisco Enterprises ltd imefanya mauzo ya Sh 2,375,310,754.61 na Kampuni ya Africa Harmony lndusry and Trade ltd imefanya mauzo ya Sh 1,929240,063.00.

Wakili Tumpale alidai wakati wa uchunguzi ilibainika zaidi kuwa watuhumiwa wote wanne walikuwa wakiongoza na kuratibu genge la uhalifu wa makosa mbalimbali ambayo ni kutoa risiti zisizo sahihi, kutumia mashine za kieletroniki kwa namna ya kuupotosha mfumo au Kamishna Mkuu wa TRA, kukwepa kodi kinyume na sheria, kuisababishia hasara TRA na kutakatisha fedha.

Anadai kuwa washitakiwa wote walifikishwa mahakama hiyo kujibu mashitaka yanayowakabili.

Baada ya kusomewa hoja za awali, washitakiwa wote walikiri majina yao, maeneo wanayoishi na kufikishwa mahakamani hata hivyo, walikana mashtaka yote.

Mshtakiwa Mhavile alikana dini iliyoandikwa kwamba ni mkristu akidai yeye ni muislamu, pia alikana kuwa fundi wa mashine za kielektroniki na kueleza kuwa yeye ni msambazaji wa mashine hizo.

Hakimu Kuppa ameahirisha shauri hilo hadi Septemba 24, mwaka huu kwa ajili ya kuanza kusikilizwa.

Washtakiwa walirudishwa rumande kwa kuwa mashitaka yanayowakabili hayana dhamana.

 
Jaji Mkuu wa Tanzania na Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Mahakama, Prof. Ibrahim Hamis Juma Kushoto akimuapisha Mwanasheria Mkuu wa Serikali  Hamza Johari kuwa Kamishna wa Tume ya Utumishi wa Mahakama Septemba 07, 2024 jijini Dar es salaam.

Jaji Mkuu wa Tanzania na Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Mahakama Prof. Ibrahim, Hamis Juma akizungumza mara baada ya kumuapisha Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Hamza Johari kuwa Kamishna wa TumeTume ya Utumishi wa Mahakama Septemba 07, 2024 jijini Dar es salaam.
Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Hamza Johari akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kuapishwa kuwa Kamishna wa TumeTume ya Utumishi wa Mahakama Septemba 07, 2024 jijini Dar es salaam.



Picha ya pamoja.

Na Avila Kakingo, Michuzi Tv
MWANASHERIA Mkuu wa Serikali ni mtu muhimu sana sio tu kwa mahakama bali Bunge na serikali na pengine ndio maana hula viapo vitatu ikionesha umuhimu wa nafasi yake.

Hayo yamesemwa leo Septemba 07, 2024 na Jaji Mkuu Profesa Ibrahim Hamis Juma wakati wa kumuapisha Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Hamza Johari kuwa Kamishna n mjumbe wa Tume ya Utumishi wa Mahakama.

Amesema kuwa ndio maana anakula viapo vitatu, ambapo ni viongozi wachache sana wanakula viapo vingi zaidi kuliko wengine.

"Hii inaonesha umuhimu wa nafasi yake kutokana na kuwa mtetezi mkuu wa Mahakama mara nyingi watu huwa hawauoni umuhimu wake ...." 

Prof. Juma amesema kuwa kama kunatokea mkwaruzano wowote na kiongozi wa muhimili mwingine au akivuka anga na kuingia kwenye anga la Mahakama kwa kutokujua amesema wananjia nyingi za mashauriano kwa kutumia Mwanasheria mkuu wa Serikali kufikisha ujumbe na kuelimishana kwamba hayo simajukumu yake ni majukumu ya watu wengine kwa kufanya hivyo kumesaidia.

"Aliyevuka anga akielimishwa anashukuru sana anasema nilikuwa sijui kwamba hii anga nilikuwa sitakiwi kufika. Hizo ndio kazi kuu kwani anakuwa mtetezi wa mahakama na ametusaidia sana."

Pia Prof. Juma amemuasa ahakikishe anafahamu kila kitu kinachoendelea ndani ya mihimili ya serikali lakini pia twatatoa ushirikiano kwenye kila kitu muhimu, kama kuna nyaraka muhimu zimetoka, sera   ni muhimu aelewe, kwani hajui taarifa zitaenda kutumika wapi.

Kwa upande wa Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania na aliyekuwa  Mwanasheria Mkuu wa Serikali,  Dkt. Eliezer Feleshi, amesema kuwa wana matumaini makubwa na Mwanasheria huyo katika usimaizi wa sheria. 

"Nafasi ya Mwanasheria Mkuu wa serikali ni nafasi ya pekee, anaiwezesha tume kuwa na afisa ambaye kwa dhamana yake anaingia akiwa na uwakilishi kwenye mihimili mingine ya serikali, yeye yupo serikalini anaingia kwenye mabaraza mengi na anaelewa nini kinaendelea Serikalini lakini pia anapoingia bungeni anahakikisha hakuna Matope. 

Pia asema kuwa atampa ushirikiano wa kutosha kwa kufanya kazi kwa ufanisi na  kumwezesha kufanya kazi kwa umahiri zaidi.

 Kwa upande wa  Mwanasheria mkuu wa Serikali, Hamza Johari amesema kuwa anatambua kuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali ni daraja katika mihimili mitatu ya serikali.

Pia amesema atajitajidi kufanya kazi kwa pamoja, na kuhakikisha kwamba malengo ambayo watajiwekea watayatimiza.

"Nilazima sasa kama Ofisi ya Mwanasheria mkuu wa Serikali tuhakikishe kwamba tunatekeleza majukumu yetu ipasavyo na ule ushiriki wetu katika maeneo yote yanayohitaji mchango tutafanya hivyo kwa weledi lakini pia kwaharaka kutoa huduma ambazo ni bora na zenye tija kwa Taifa letu." Amesema Johari