Na Ibrahim Mdachi, Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto
Chuo Cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) kimeitisha kongamano maalum
la wadau, kupitia na kutolea maoni mtaala wa mafunzo elekezi kwa Mawakili na
Wanasheria wa Sekta ya Umma. Akizindua kongamano hilo jijini Dodoma, mwishoni mwa wiki iliyopita kwa niaba
ya Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala
Bora, Bw. Mick Kiliba, alisema kwa ujumla mafunzo yatakayotolewa na IJA
yanalenga kujenga uwezo kwa wanasheria wapya wa Serikali.
Bw. Kiliba alisema kuwa Mafunzo hayo yanalenga kujua mifumo ya uendeshaji
wa shughuli za kiserikali, uongozi na utumishi wa umma. Kwa lengo la kuwaandaa
waajiriwa wapya wa kada ya sheria kutoa utumishi ulio bora na uliotukuka.
Alisema kuwa, matarajio ya Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utawala Bora kupitia
Mafunzo haya ni kuona kila Mwanasheria aliyeajiriwa katika Utumishi wa Umma
anafahamu ipasavyo; majukumu yake ya kazi. Aliongeza kuwa ni wajibu wa Mwanasheria kujua wajibu wake kama Mtumishi wa
Umma, Muundo wa Serikali na Utunzaji wa siri za Serikali hali kadhalika kuiva
kimaadili na kinidhamu.
“Itakumbukwa kuwa, waraka Na.5 wa mwaka 2011 wa Ofisi ya Rais Menejimenti
ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, unaelekeza kutolewa kwa mafunzo
elekezi kwa Watumishi wapya katika Utumishi wa Umma,” alieleza.
Aidha, kongamano hili ni utekelezaji wa Mpango Mkakati wa Miaka Mitano wa
Chuo cha IJA wa 2018/19 - 2022/23 ambapo Chuo cha IJA kilishirikiana na Wataalamu kutoka Wizara ya Katiba na Sheria, Ofisi ya Rais Menejimenti ya
Utumishi wa Umma na Utawala Bora, pamoja na wadau mbalimbali wa sekta ya
Umma kama vile Mahakama ya Tanzania na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa
Serikali. Miongoni mwa masuala muhimu yanayoangaziwa katika mtaala huo ni pamoja na
kuwawezesha waajiriwa wapya kuelewa namna ya kuendesha shughuli za serikali,
kuelewa sheria, kanuni na taratibu katika Utumishi wa Umma.
Chuo cha IJA kimekasimiwa madaraka ya kuandaa na kutoa mafunzo ya awali na
elekezi kwa waajiriwa wote wa kada ya sheria katika sekta ya Umma nchini.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...