Watendaji Wakuu katika Taasisi
za Umma nchini wametakiwa kutekeleza kwa vitendo kauli mbiu ya HAPA
KAZI TU ya Mhe. Rais, Dkt. John Pombe Magufuli, kwa kuhakikisha
wanasimamia vizuri utekelezaji wa Mfumo wa Wazi wa Mapitio na Tathmini
ya Utendaji Kazi (OPRAS) wa mtumishi mmoja mmoja ili kuongeza ufanisi
katika utendaji kazi kwa maslahi ya maendeleo ya taifa.
Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa
Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora,
Mhe. Dkt. Mary Mwanjelwa alipoitembelea Idara ya Mikataba ya Utendaji
Kazi Serikalini ya Ofisi yake kwa lengo la kufahamu majukumu ya idara
hiyo na kuhimiza uwajibikaji.
Mhe. Dkt. Mwanjelwa amesema,
usimamizi na utekelezaji mzuri wa Mfumo wa Wazi wa Mapitio na Tathmini
ya Utendaji Kazi (OPRAS) utaondoa tatizo la ufanyaji kazi wa mazoea kwa
baadhi ya watumishi wa umma nchini na kuongeza kuwa, utawezesha kufikia
azma ya Serikali ya Awamu ya Tano ya kujenga utamaduni wa kila mtumishi
wa umma katika nafasi aliyonayo kufanya kazi kwa bidii, ufanisi na
weledi ili utumishi wake uwe na tija katika maendeleo ya taifa.
Mhe. Dkt. Mwanjelwa amesisitiza
kuwa, Serikali ya Awamu ya Tano inataka kuwa na OPRAS ambayo ni chachu
ya kuimarisha utendaji kazi na uwajibikaji kwa kila mtumishi wa umma,
hivyo ameitaka Idara ya Mikataba ya Utendaji Kazi Serikalini ambayo ina
majukumu la kutoa miongozo na kusimamia OPRAS, kuweka msingi imara wa
usimamizi na utekelezaji wa OPRAS katika Taasisi za Umma.
Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Dkt. Mary Mwanjelwa (Mb) akizungumza na watumishi wa Idara ya Mikataba ya Utendaji Kazi Serikalini wa Ofisi yake kuhusu utekelezaji wa Mfumo wa Wazi wa Mapitio na Tathmini ya Utendaji Kazi (OPRAS) kwa watumishi wa umma, alipoitembelea Idara hiyo kwa lengo la kufahamu majukumu ya idara na kuhimiza uwajibikaji.
Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Dkt. Mary Mwanjelwa (Mb) akielezwa majukumu ya Idara ya Mikataba ya Utendaji Kazi Serikalini na mkurugenzi wa Idara hiyo, Bw. Hassan Kitenge, alipoitembelea Idara hiyo kwa lengo la kufahamu majukumu ya idara na kuhimiza uwajibikaji.
Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Dkt. Mary Mwanjelwa (Mb) akihimiza usimamizi mzuri wa Mfumo wa Wazi wa Mapitio na Tathmini ya Utendaji Kazi (OPRAS) kwa Mkurugenzi wa Idara ya Mikataba ya Utendaji Kazi Serikalini, Bw. Hassan Kitenge, alipoitembelea Idara hiyo kwa lengo la kufahamu majukumu ya idara na kuhimiza uwajibikaji.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...