Serikali iko katika mpango wa kujenga Kituo cha Polisi katika Halmashauri ya Itigi ikiwa ni juhudi za kulinda hujuma na uhalifu katika Ujenzi wa Reli ya Kisasa (Standard Gauge) na Mradi wa Umeme katika maporomoko ya maji ya Mto Rufiji (Stiegler’s Gorge) baada ya wavamizi kuingia eneo la hifadhi ya Rungwa ambayo kuna mito 18 ambayo ni chanzo cha Mto Rufiji ambako mradi wa umeme unajengwa. 

Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhandisi Hamad Masauni akitembelea na kukagua Mradi wa Kituo kipya cha Polisi cha Wilaya ya Manyoni na kukagua eneo linarotarajiwa kujengwa Kituo cha Polisi Itigi lengo ikiwa kudhibiti matukio ya uhalifu. 

Akiambatana na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Manyoni, Naibu Waziri Masauni amesema Serikali iko tayari kutumia mbinu mbalimbali kuhakikisha miradi mikubwa ambayo Serikali ya Awamu ya Tano imeianza inakamilika bila kufanyiwa hujuma zozote na wahalifu. 

“Miradi mikubwa ambayo Rais wetu Dkt. John Magufuli na serikali anayoiongoza ameianzisha ni muhimu ikalindwa ili ilete manufaa kwa nchi pindi itakapokamilika na sisi kama wizara tutahakikisha tunasogeza huduma za Ulinzi na Usalama katika maeneo yote ambayo miradi hiyo inapitia, ndio maana leo nimetembelea ujenzi wa Kituo cha Polisi Manyoni ambacho kiko mbioni kukamilika lengo ikiwa ni kulinda miradi hiyo mikubwa,” alisema Masauni 

Akizungumza katika ziara hiyo, Mbunge wa Jimbo la Manyoni Mashariki, Daniel Mtuka amekiri kuwepo na haja ya kituo katika Wilaya za Manyoni na Itigi ili kuweza kuboresha usalama katika maeneo hayo ambayo yanapitiwa na miradi hiyo mikubwa miwili huku akiiomba wizara kuleta askari katika vituo hivy pindi ujenzi utakapokamilika. 
Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhandisi Hamad Masauni, akizungumza katika kikao cha ndani kilichojumuisha Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Manyoni wakati wa ziara ya kikazi, lengo ikiwa ni kuweka mikakati ya kudhibiti hujuma na uhalifu katika maeneo inapopita miradi mbalimbali ya serikali. Naibu Waziri yuko mkoani Singida kwa ziara ya kikazi.
Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhandisi Hamad Masauni(wapili kushoto), akiangalia ramani ya eneo linarotarajiwa kuejngwa kituo cha Jeshi la Zimamoto na Uokoaji.Wengine ni Wajumbe wa Kamati ya Ulinzi na Usalama wilayani Manyoni Naibu Waziri yuko mkoani Singida kwa ziara ya kikazi.
Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhandisi Hamad Masauni (katikati mstari wa mbele), akiongozana na Wajumbe wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Manyoni kuingia katika Kituo cha Polisi cha Manyoni kinachojengwa baada ya kituo cha awali kupitiwa na Mradi wa Ujenzi wa Reli ya Kisasa . Naibu Waziri yuko mkoani Singida kwa ziara ya kikazi. 
Muonekano wa nje Kituo Kipya cha Polisi Wilaya ya Manyoni ambacho kipo mbioni kukamilika ambacho kinategemewa kudhibiti hujuma na uhalifu katika maeneo mbalimbali inakopita miradi mikubwa ya serikali .Picha na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi 

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...