Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi
Mhe. Abdallah Ulega akipata maelezo ya mashine zinazofungwa kwenye
kiwanda kutoka kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Kiwanda cha Ace Leather Bw.
Onorato Garavaglia
Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi
Mhe. Abdallah Ulega (katikati) akikagua na kupata maelezo ya mashine
zinazofungwa kwenye kiwanda cha Ace Leather.
*********************************
Na. Edward Kondela
Naibu Waziri wa
Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega amesema wizara yake itahakikisha
matamanio ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Magufuli
ya nchi kuuza ngozi na bidhaa zake kwenda nchi za nje yanafikiwa.
Akizungumza
mwishoni mwa wiki wakati alipotembelea Kiwanda cha kuchakata ngozi cha
Ace Leather kilichopo katika Manispaa ya Morogoro na kujionea maboresho
makubwa ya kiwanda hicho kwa kufungwa mashine za kisasa, Mhe. Ulega
amesema wizara itahakikisha pia uwezekano wa kupunguza gharama kununua
bidhaa za ngozi kutoka nchi za nje kuja hapa nchini zinapunguzwa.
“Matamanio ya
serikali ya Rais Magufuli kila mara amekuwa akizungumzia kuhusu zao la
ngozi, nchi yetu ina mifugo mingi sana na kila mara matamanio yake kuona
Tanzania haitumii tena gharama kubwa kununua bidhaa za ngozi kutoka
katika mataifa ya nje bali sisi ndiyo tuwauzie ngozi na bidhaa zake.” Amesema Mhe. Ulega
Aidha Mhe. Ulega
amesema ameridhishwa na mitambo ya kisasa inayofungwa katika Kiwanda cha
Ace Leather ambacho kinatarajiwa kufunguliwa tena hivi karibuni baada
ya kusitisha shughuli zake ili kupisha maboresho ya kiwanda hicho kwa
kufungwa mitambo hiyo ya kisasa.
Kwa upande wake
Makamu Mwenyekiti wa makampuni ya Taifa Group of Companies inayomiliki
kiwanda hicho Bw. Abdulkarim Shah amesema mara baada ya kiwanda hicho
kukamilika maboresho yake kitakuwa ni moja ya viwanda vikubwa katika
ukanda wa kusini mwa janga la sahara.
Bw. Shah amesema
mara baada ya kiwanda hicho kukamilika kinatarajiwa kuajiri takriban
wafanyakazi 250 hadi 300 na nia ya kiwanda hicho katika siku zijazo ni
kuanza kutengeneza bidhaa za ngozi.
Katika hatua
nyingine Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega amekagua
pia ujenzi wa kiwanda cha kuchakata nyama cha Nguru Hills kilichopo
katika Wilaya ya Mvomero Mkoani Morogoro ambapo amesema ameridhishwa na
ujenzi wa kiwanda hicho.
Kufuatia ujenzi
wa viwanda vya kuchakata nyama vinavyojengwa maeneo mbalimbali hapa
nchini, Naibu Waziri Ulega amehamasisha wananchi kufanya biashara ya
kunenepesha mifugo kwa kuwa viwanda hivyo mara vitakapokamilika
vitahitaji mifugo mingi kwa ajili ya uchakataji.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...