Mwenyekiti wa Wachimbaji wa Madini Mkoa wa Mbeya, Leonard Manyesha (aliyesimama), akiongea wakati wa Mkutano wa viongozi wa wachimbaji wa madini ya dhahabu Wilaya ya Chunya na viongozi kutoka Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali ambao ni Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi na Mkemia Mkuu wa Serikali (hawapo pichani).
Mkemia Mkuu wa Serikali, Dkt. Fidelice Mafumiko (aliyesimama), akiongea na viongozi hao wa wachimbaji wa madini ya dhahabu Wilaya ya Chunya (hawapo Pichani) katika Mkutano huo uliofanyika wilayani Chunya.

Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali, Profesa Esther Hellen Jason (wa pili kulia) akiongea na viongozi wa wachimbaji wa dhahabu katika migodi ya Chunya (hawapo pichani). Mwenyekiti wa Bodi na Mkemia Mkuu wa Serikali (wa tatu kulia), walikutana na wadau hao kwa lengo la kuwasikiliza maoni waliyonayo juu ya huduma zinazotolewa na Mamlaka hiyo

Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi, Profesa Esther Hellen Jason (aliyekaa katikati), Mkemia Mkuu wa Serikali, Dkt. Fidelice Mafumiko (wa pili kushoto), wakiwa pamoja na Mwenyekiti wa Wachimbaji wa Dhahabu Mkoa wa Mbeya, Leonard Manyesha (wa pili kulia), Kaimu Meneja wa Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali, Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, Gaspar Mushi (kulia) na viongozi wengine wa wachimbaji  na wamiliki migodi ya dhahabu iliyopo katika Wilaya ya Chunya.

*****************************
Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali, Prof. Esther Hellen Jason amewataka wachimbaji wa madini ya dhahabu wa Chunya kuzingatia matumizi salama ya kemikali wanazozitumia katika shughuli zao za uchimbaji kwa lengo la kulinda afya na mazingira.

Prof. Esther Hellen Jason ameyasema hayo wilayani Chunya wakati akiongea na viongozi wa wachimbaji na wamiliki wa migodi ya madini ya dhahabu.
“Ndugu zangu tuzingatie matumizi salama ya kemikali kwa lengo la kulinda mazingira, afya zetu na vizazi vyetu, tunatambua sekta ya madini ni moja ya sekta muhimu sana katika kukuza uchumi wa nchi kwa sababu dhahabu inaingiza mapato ndani ya Serikali lakini huwezi kuipata dhahabu bila kutumia baadhi ya kemikali.” Alisema Prof. Jason.

Ameongeza kuwa, kukutana na wadau na kujadiliana namna bora ya kuimarisha mahusiano ya kikazi ni njia sahihi ya kutatua changamoto na kuboresha utendaji kazi wa pande zote katika shughuli hizi za uchimbaji na uchenjuaji wa dhahabu.
Hivyo changamoto zenu mlizowasilisha leo tunazichukua kwa uzito mkubwa na tutayafanyia kazi ili kuboresha zaidi utendaji wetu na shughuli zenu.

“Kwa zile zilizo ndani ya uwezo wa Bodi ya Wakurugenzi tutazifanyia kazi kwa lengo la kurahisisha utendaji wenu na zinayohitaji maamuzi ya juu zaidi tutayawasilisha ili kupatiwa ufumbuzi maana zikitatuliwa changamoto hizi tunaamini hazitakuwa kwa faida ya Chunya tu bali kwa wachimbaji wa Tanzania nzima wanaotumia kemikali.” Alimalizia

Kwa upande wake, Mkemia Mkuu wa Serikali, Dkt. Fidelice Mafumiko, alisema mkutano huo ni mwanzo wa ushirikiano wa Mamlaka na wachimbaji hao wenye lengo la kutatua changamoto na kuzifanya kuwa fursa za kuboresha utendaji na kuwezesha wadau hao wa Chunya na maeneo mengine ya migodi nchini.
  Akiongea kwa niaba ya wachimbaji, Mwenyekiti wa Wachimbaji wa dhahabu Mkoa wa Mbeya, Leonard Manyesha, alisema anashukuru kwa mkutano huo na anaamini mazuri yaliyojadiliwa yataleta tija yakifanyiwa kazi.

“Nimefurahishwa na mkutano huu na naamini tuliyojadili yakifanyiwa kazi yataleta tija kwenye kazi zetu za uchimbaji wa dhahabu. Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali wamekuwa karibu sana kwetu hasa kwenye mafunzo ya matumizi salama ya kemikali na kutatua changamoto zetu pale tunapoziwasilisha.” Alisema Manyesha.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...