Picha ya pamoja ikionyesha washiriki wa zoezi la mahakama mtandao katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu na Gereza la Keko jijini Dar es Salaam.
Maafisa wa magereza wakifuatilia mashauri kwa njia Mahakama Mtandao (kushoto) Musa Kaswaka na (kulia) kwake ni George Mwambashi yaliyokuwa yakiendeshwa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam.
Baadhi ya wananchi waliofika katika ukumbi wa mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, iliyopo jijini Dar es Salaam wakifuatilia mwenendo wa uendeshaji mashauri kwa njia ya Mahakama Mtandao.
 
Na Innocent Kansha na Salum Tawani

Mahakama ya Hakimu  Mkazi Kisutu iliyopo Jijini Dar es Salaam leo kwa mara ya kwanza imetoa dhamana ya mahabusu Bw. Abubakari Seguni aliyepo katika Gereza la Keko kwa njia ya Mahakama Mtandao maarufu kama ‘Video Conference’.

Dhamana hiyo imetolewa na Mahakama hiyo kwa kushirikiana na Gereza la Keko lilipo katika jiji hilo, wakati ilipokuwa ikiendesha mashauri nane (8) kwa njia ya hiyo ikiwa ni mwendelezo.

Mtuhumiwa huyo namba tatu ambaye anakabiliwa na tuhuma ya rushwa na uhujumu uchumi katika shauri namba 43 la mwaka 2017 la jinai, akiwa na wenzake watano dhidi ya Serikali. Shauri hilo liletwa mahakamani hapo kwa ajili ya kutajwa.

Awali Mwendesha Mashtaka Wakili wa Serikali, Bi. Ester Martin alidai kuwa shauri hilo halijakamilika kwa sababu upelelezi wake haujakamilika na linasubiri kibali kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka nchini (DPP).

Akisoma masharti ya dhamana mahabusu huyo, Hakimu Mkazi Mwandamizi Mhe. Augustina Mmbando alieleza dhamana ya mshitakiwa ipo wazi kwa kuwa na wadhamini wawili watakao weka ahadi ya shilingi milioni Sitini (ml. 60) na mmoja kati yao lazima awe mtumishi wa Umma na kwa pamoja wawasilishe mahakamani hati zao za kusafiria.

Akiahirisha shauri hilo, Mhe. Mmbando alisema litatajwa tena Januari 2, mwaka huu saa tatu kamili asubuhi.

Mashauri mengine saba ya jinai yaliyosikilizwa kwa njia hiyo, ambayo yako katika hatua ya awali ya kutajwa yote yalihusu Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi, kama inavyoelekeza Sheria Namba Tatu ya mwaka 2016 iliyofanya mabadiliko ya Sheria ya Uhujumu Uchumi Sura namba 200, ambayo upelelezi wake haujakamilika na mengine yakisubiri kibali kutoka kwa DPP.

Ambapo shauri la kwanza lilikuwa linamhusu mtuhumiwa Eke Bidi dhidi ya Serikali, watuhumiwa wengine ni Wolfgang Sylivester, Xiao Shaudan, Hariri Hariri na wenzake, Mohamed Ismail Sued na wenzake, Ally Anguzuu Sharifu na wenzake, Maarifa Abbas Nassor na wenzake na Mohamed Mohamed, wakiwemo wenzake watano wote dhidi ya serikali.

Mashauri hayo yote yatatajwa tena Januari 27, mwaka huu.

Mmoja wa wananchi waliofika mahakamani hapo kusikiliza shauri la ndugu yake, Bw. Rajabu Bakari mkazi wa Kongowe alisema teknolojia ya Mahakama Mtandao ni nzuri ila angependa kumwona ndugu yake uso kwa uso.

Mashauri hayo yenye mahabusu 24 yameendendeshwa mahakamani hapo kupitia gereza hilo kufikia 10, ambapo mawili yaliendeshwa wiki iliyopita Januari 10, mwaka huu.

Uendeshaji wa mashauri kwa njia hiyo ni mojawapo ya malengo ya Mahakama ya Tanzania ya kuweza kusikiliza mashauri kwa wakati na kupunguza gharama za uendeshaji wa mashauri hayo mfano kuwalipa mashahidi, kuwasafirisha mahabusu, usalama wa mahabusu , zikiwemo nyingine.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...