Na Karama Kenyunko,Michuzi Globu ya jamii

RAIA  wa Tanzania zaidi ya 55 waliokuwa wamezamia nchini Afrika Kusini, wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu na kati yao 22 wamehukumiwa kutumikia kifungo cha miezi sita gerezani  baada ya kukiri kosa la kutoka nchini bila kufuata taratibu za kisheria.

Washitakiwa hao ni Mzuzuri Mohammed, Mohammed Said, Masoro Musa, Mneke Mehra, Kibila Husein, Ali Hassan, Jamalino Rashid, Abdul Nassoro, Waziru Adam na Said Salum, Chuwa Sadick, Salum Kasimum, Macalot Alex, Kayenga Winston, Idali Charles, Ibrahim Mohammed, Jafari Zebra, Omane Fizo, Mbona Edson, Ulembo Azide, Fizo Charles na Mnangwa Rajab.

Akiwasomea adhabu, Hakimu Mkazi, Vick Mwaikambo amesema anawatia hatiani washtakiwa hao kwa kuondoka nchini bila kufuata sheria za uhamiaji na kwamba akiwaangalia wote ni vijana wenye nguvu na ambao wangeweza kufanya kazi za kujenga Taifa badala ya kutorokea nje ya nchi ambako wanakuwa ni wahamiaji haramu ambao wanalitia taifa letu aibu.

Amesema kitendo cha washtakiwa hao sio cha kwanza hapa nchini, kimekuwa kikijirudia rudia mara kwa hivyo, wameliingizia Taifa gharama kwa kukodi ndege ya kuweza kuwarudisha nchini wakati fedha hizo zingeweza kujengea hospitali na kufanya shughuli nyingine za maendeleo.

"Makosa haya yamekuwa yakijirudia hivyo Mahakama hii inawapa adhabu ya kifungo cha miezi sita jela bila faini na mkafanye kazi mbalimbali mtakazopangiwa na magereza," amesema Hakimu Mwaikambo.

Kabla ya kutolewa kwa adhabu hiyo, Wakili wa Serikali, Shija Sitta aliiomba Mahakama kutoa adhabu kali kwa washitakiwa ili iwe fundisho kwa vijana wengine na kudai kuwa taratibu za kusafiri nje ya nchi zipo na kwamba hakuna msingi wa watu kwenda Afrika Kusini bila kibali kitendo ambacho kimezalilisha taifa kwa kuonekana ni wahamiaji haramu.

Washitakiwa hao kwa nyakati tofauti waliiomba mahakama iwapunguzie adhabu ili kulitumikia taifa.

Awali, akisoma mashtka,  Wakili Sitta alidai washitakiwa hao walitoka nje ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kinyume  na kanuni za uhamiaji namba 20 (3) (a)  G.N namba 657 ya mwaka 1997 inayosomwa pamoja na kifungu namba 48 (2) ya Sheria ya Uhamiaji namba 54 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2016.

Alidai Januari 21, mwaka huu maeneo ya Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), washitakiwa hao wakiwa raia wa Tanzania walikutwa wakiwa wametoka nje ya nchi bila kufuata utaratibu wa kutoka nchini kwenda Afrika Kusini kwa kupitia mipaka inayojulikana.

Washitakiwa wote wamekubali mashitaka hayo na upande wa mashtaka uliwasomea maelezo ya awali ambapo wakili wa serikali Godfrey Ngwijo alidai tarehe zisizofahamika walitoka Tanzania na kuingia Afrika Kusini bila kufuata taratibu.

Ngwijo alidai katika tarehe hiyo, washitakiwa walikamatwa nchini Afrika Kusini na kuletwa Tanzania na kwamba walifikishwa kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere na kwamba walipelekwa Ofisi ya Mkoa wa Dar es Salaam na kuchukuliwa maelezo.

Aidha washtakiwa wengine 18,  wamesomewa mashtaka yao mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Salim Ally  na wamehukumiwa kifungo cha miezi 18 jela ama kulipa faini ya sh. Elfu 50.

Washtakiwa hao  ni, Adul Zuberi, Rajab Kassim, Rashid Yasin, Mussa Twahir, Twaha Sherif,  Mbaruku Amran, Kuambiana Ally, Khaulusha Said, Ladu Mukapa, Juma Sharan, Ramadhani Issa, Amadi Katundi, Mapunda Cosmas, Mwinshehe Hassan, Dotto Nyungwa, Asann Mohamed, Winfred George na Tikoini.

Hata hivyo, mahakama hawakuweza kuwasomewa washtakiwa wengine 19 mashtaka yao  hadi Januari 27, 2020 (Jumatatu) kwa sababu hakimu Augustina Mmbando aliyepaswa kusikiliza kesi yao amepata udhuru.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

Kuna Maoni 1 mpaka sasa

  1. Hebu fungeni mafisadi ambao hatuwaoni magerezani. Sio raia wema inaowalazimu kutoka nje ya nchi kwenda kutafuta maisha kutokana na kukosa matumaini nchini kwao.

    ReplyDelete

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...