Serikali itaendelea kushirikiana kwa karibu na wawekezaji wa sekta ya viwanda ili kutatua changamoto zinazokwamisha uzalishaji na kuweka mazingira bora yatakayochochea ukuaji wa uchumi wa viwanda nchini.

Kauli hiyo imetolewa  na  Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe.Judith Kapinga mara baada ya kufanya ziara katika kiwanda kikubwa cha kuchakata na kuzalisha mafuta ya kula cha Mainland Group Agro Process Tanzania  jijini Dodoma, ambapo amejionea shughuli mbalimbali za uzalishaji na kiwango cha uwekezaji kilichofanyika katika kiwanda hicho.

Akizungumza baada ya kutembelea mitambo ya uzalishaji, Waziri Kapinga amesema   Serikali inatambua mchango mkubwa wa sekta binafsi katika kukuza uchumi, kuongeza ajira na kuimarisha mapato ya Taifa, hivyo itaendelea kuhakikisha changamoto zinazowakabili wawekezaji zinapatiwa ufumbuzi kwa wakati.

Amesema ameoneshwa kuvutiwa na uwekezaji mkubwa uliofanyika katika kiwanda hicho na kusisitiza kuwa viwanda vya kuongeza thamani ya mazao ya ndani vina nafasi muhimu katika kufanikisha malengo ya maendeleo ya Taifa pamoja na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

“Tunataka kuona mazao yanayozalishwa na wakulima wetu yanaongezewa thamani hapa hapa nchini. Hii ndiyo njia sahihi ya kuongeza tija kwa mkulima, mfanyabiashara, mwekezaji na Serikali kwa ujumla,” amesema Kapinga

Amebainisha kuwa licha ya Tanzania kuwa miongoni mwa wazalishaji wakubwa wa mazao ya mafuta, bado uzalishaji wa mafuta ya kula haujakidhi mahitaji ya ndani, hali inayolazimu nchi kuagiza sehemu ya mafuta kutoka nje.

Kutokana na hali hiyo, amesema Serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali ikiwemo maboresho ya sera, sheria na mifumo ya kodi ili kuvutia uwekezaji zaidi katika viwanda vya mafuta ya kula na kuongeza uzalishaji wa ndani.

Waziri huyo amesema Serikali inalenga kuona nchi inafikia kujitosheleza kwa mafuta ya kula katika miaka ijayo kwa kuongeza uzalishaji wa malighafi na kuimarisha uwezo wa viwanda vilivyopo.

Katika mazungumzo yake na viongozi wa kiwanda hicho, ameelezwa kuwa changamoto kubwa inayokikabili ni upatikanaji mdogo wa malighafi, hususan mbegu za mazao ya mafuta, jambo linalofanya kiwanda kufanya kazi chini ya uwezo wake licha ya uwekezaji mkubwa uliowekwa.

Aidha, Serikali imeanza kushirikiana na Wizara ya Kilimo pamoja na taasisi zake kuweka mikakati ya kuongeza uzalishaji wa mazao ya mafuta ili kuhakikisha viwanda vinapata malighafi za kutosha na kutumia uwezo wake kikamilifu.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa kiwanda hicho, Bw. Jiaweli Chen, ameipongeza Serikali ya Tanzania kwa kuendelea kuboresha mazingira ya uwekezaji na kutoa ushirikiano unaowezesha viwanda kufanya kazi kwa ufanisi na kuchangia maendeleo ya uchumi wa nchi.

Amesema kuwa sera na hatua mbalimbali zinazochukuliwa na Serikali zimeongeza imani kwa wawekezaji, jambo ambalo limechangia ukuaji wa shughuli za uzalishaji na kuongeza ajira kwa wananchi katika maeneo mbalimbali nchini.

Bw. Chen pia ameishukuru Serikali kwa kutembelea mradi huo na kusikiliza changamoto zinazowakabili, akieleza kuwa hatua hiyo inaonesha utayari wa viongozi kushirikiana na sekta binafsi katika kutafuta suluhisho la changamoto zinazojitokeza wakati wa utekelezaji wa shughuli za uzalishaji.

Hatahivyo amesema kuwa kiwanda hicho kitaendelea kushirikiana na Serikali katika kuongeza uzalishaji, kuimarisha ubora wa bidhaa na kuchangia jitihada za taifa za kukuza sekta ya viwanda, huku akieleza matumaini yake kuwa changamoto zilizowasilishwa zitapatiwa ufumbuzi kwa manufaa ya wawekezaji na wananchi kwa ujumla.

Na Nasra Ismail, Geita

MKURUGENZI Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Geita, Karia Rajab Magaro, Juni 25, 2026 ametembelea mradi wa ujenzi wa Soko la Kisasa Nkome Kata ya Nkome, Wilaya ya Geita. Lengo la ziara hiyo lilikuwa kujionea maendeleo ya mradi unaotarajiwa kuchochea biashara na ukuaji wa uchumi katika eneo hilo.

Akizungumza na mkandarasi wa mradi, kampuni ya RIN Contractor and General Supplies Company Ltd, Magaro amemuelekeza kuongeza kasi ya ujenzi ili mradi ukamilike na kukabidhiwa ifikapo mwishoni mwa Julai 2026 kama ilivyoelezwa kwenye mkataba.

Amesema Serikali inaendelea kusimamia kwa karibu utekelezaji wa miradi ya maendeleo ili wananchi wapate miundombinu bora inayokidhi mahitaji ya sasa na ya baadaye.

Mradi huo unafadhiliwa na Mgodi wa Dhahabu wa Geita - GGML kwa gharama ya Shilingi 473,909,792.82 hadi kukamilika. Ujenzi wa soko hilo unatarajiwa kuimarisha biashara, kuongeza ajira na kuinua kipato cha wananchi wa Nkome na maeneo jirani.

Akitoa taarifa ya maendeleo, Mhandisi wa mradi Eng. Edson Missana amesema soko hilo la kisasa litakuwa na uwezo wa kuhudumia wafanyabiashara na watumiaji zaidi ya 80 kwa wakati mmoja. Pia lina jengo la vyoo matundu 10 pamoja na mabafu maalumu kwa matumizi ya wafanyabiashara na wananchi.







-Zaidi ya Wataalamu 30 Wanufaika na mafunzo kupitia Mradi wa  Kizuna

📍 Dodoma

Serikali ya Tanzania kupitia Wizara ya Madini na Shirika la Ushirikiano wa Kimataifa la Japan (JICA) zimekubaliana kupanua wigo wa ushirikiano kwa kubainisha maeneo ya kipaumbele yatakayofadhiliwa kupitia JICA kwa msaada wa Serikali ya Japan ikiwemo utafiti wa madini muhimu na mkakati.

Hayo yamebainishwa Juni 25, 2026 jijini Dodoma katika kikao kilicholenga kuimarisha ushirikiano katika maendeleo ya Sekta ya Madini nchini.

Akizungumza katika kikao hicho, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Madini Msafiri Mbibo amesema ushirikiano na taasisi hiyo ni wa muda mrefu ambao kupitia JICA zaidi ya wataalamu 30 wa Sekta ya Madini wamepatiwa mafunzo nchini Japan yaliyowajengea uwezo na kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu ya Wizara na taasisi zake na kueleza kwamba, ushirikiano huo utaendelea kuimarishwa kwa manufaa ya Tanzania na Japan.

Kwa upande wake, Mwakilishi Mkazi wa JICA nchini Tanzania, Dkt. Katsuyika Kuge, amesema pamoja na utekelezaji wa Mradi wa Kizuna unaojenga uwezo wa wataalamu wa sekta hiyo, JICA inapanga kupanua ushirikiano katika maeneo ya utafiti wa madini muhimu na madini mkakati, ikiwemo shaba, kinywe (graphite), beryllium na madini adimu ya Heavy Rare Earth Elements (Heavy REE). 

Aidha, Dkt. amefafanua kuwa, kwa kuanzingatia vipaumbele vya JICA, kwa kuanzia,  kipaumbele  cha utafiti kitajikita kwenye eneo la madini kinywe na beryllium.

‘’ Ninaipongeza Serikali ya Tanzania kwa usimamizi mzuri wa Sekta ya Madini, pamoja na utekelezaji wa mradi wa Kizuna unaowajengea uwezo watalaam wa Sekta ya madini, JICA inapanga kupanua ushirikiano katika maeneo ya utafiti wa madini muhimu na mkakati,’’ amesema Dkt.Kuge.






-Uchumi wa Bluu Kunufaika na Elimu ya Ubaharia

Na Mwandishi Wetu, Kigoma

Waziri wa Uchukuzi, Profesa Makame Mnyaa Mbarawa, amesema Serikali itaendelea kukiunga mkono Chuo cha Bahari Dar es Salaam (DMI) katika jitihada zake za kuanzisha kozi ya awali ya ubaharia itakayowawezesha vijana wengi zaidi wa Kitanzania kupata elimu ya sekta hiyo na kushiriki kikamilifu katika kukuza uchumi wa bluu.

Profesa Mbarawa ametoa kauli hiyo alipotembelea banda la DMI katika kilele cha Maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani yaliyofanyika mkoani Kigoma, ambapo alieleza kuwa kozi hiyo ni suluhisho kwa vijana wengi wenye ndoto za kuwa mabaharia lakini ambao hawakupata nafasi ya kusoma masomo ya sayansi yanayohitajika kujiunga na taaluma hiyo.

Alisema DMI imebuni mpango huo mahsusi ili kuwapa vijana hao fursa ya kupata msingi wa masomo muhimu yatakayowawezesha kuendelea na mafunzo ya ubaharia na hatimaye kuingia katika soko la ajira la sekta ya usafiri wa majini.

“DMI inafanya kazi kubwa ya kuangalia namna ya kuwawezesha vijana wengi zaidi kupata fursa za elimu ya ubaharia. Kozi hii ya awali itawasaidia wale ambao hawakusoma masomo ya sayansi kupata msingi unaohitajika na hatimaye kujiunga na mafunzo ya ubaharia,” alisema Profesa Mbarawa.

Alibainisha kuwa hatua hiyo ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kuongeza idadi ya mabaharia wenye ujuzi na sifa zinazotambulika kitaifa na kimataifa, huku ikilenga kuongeza ushiriki wa Watanzania katika ajira za sekta ya bahari na usafiri wa majini duniani.

Waziri huyo pia alimpongeza Mkuu wa Chuo cha DMI, Profesa Tumaini Gurumo, kwa ubunifu na juhudi zake za kuendeleza programu mbalimbali za mafunzo zinazowawezesha mabaharia wa Tanzania kufikia viwango vya kimataifa vinavyohitajika katika sekta ya usafiri wa majini.

“Tunakipongeza DMI kwa juhudi zake za kubuni na kuendeleza mafunzo yanayowawezesha mabaharia wetu kuwa na sifa zinazokubalika kimataifa. Mabaharia wanazunguka dunia nzima, hivyo ni lazima waandaliwe kwa viwango vinavyokidhi mahitaji ya sekta ya kimataifa,” alisema Profesa Mbarawa.

Kwa upande wake, Mkuu wa Chuo cha DMI, Profesa Tumaini Gurumo, ameishukuru Serikali kupitia Wizara ya Uchukuzi kwa kuendelea kukiunga mkono chuo hicho katika kuzalisha wataalamu wenye tija na ushindani katika soko la ajira la ndani na nje ya nchi.

Profesa Gurumo alisema kutokana na asili ya kazi ya ubaharia inayowafanya mabaharia kufanya kazi na kusafiri katika mataifa mbalimbali duniani, ni muhimu kwao kupata elimu na stadi zinazotambulika kimataifa ili waweze kushindana kwa ufanisi katika soko la ajira la dunia.

Aliongeza kuwa DMI itaendelea kupanua na kuboresha mafunzo ya bahari ili kuhakikisha vijana wengi zaidi wanapata elimu na ujuzi unaohitajika kwa taifa kunufaika na fursa zilizopo katika uchumi wa bluu na sekta ya usafiri wa majini.

Maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani yamewakutanisha wadau mbalimbali wa sekta ya bahari na usafiri wa majini kwa lengo la kutambua na kuthamini mchango mkubwa wa mabaharia katika kukuza biashara, uchumi na maendeleo ya jamii duniani.



Matukio ya picha ya Waziri Profesa Mbarawa katika Banda la DMI,Kigoma

Na Janeth Raphael-MichuziTv


Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) limeahidi kuchangia fedha kwa ajili ya kuimarisha huduma za upandikizaji figo na uroto (selimundu) katika Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH), ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za Serikali za kuboresha huduma za afya nchini kuelekea maadhimisho ya miaka 10 ya hospitali hiyo yanayotarajiwa kufanyika Julai 15, 2026.

Akizungumza wakati wa ziara ya wahariri wa vyombo mbalimballi vya habari nchini katika hospitali hiyo jijini Dodoma, Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania, Deodatus Balile, amesema mchango huo unalenga kusaidia wagonjwa wasiokuwa na uwezo wa kugharamia matibabu ya kibingwa yanayotolewa na hospitali hiyo.

Balile amesema huduma za kibingwa zinazopatikana BMH zimekuwa mkombozi kwa Watanzania wengi kutokana na ubora wake na gharama nafuu ikilinganishwa na matibabu yanayopatikana nje ya nchi.

“Hakuna mtu ambaye hapendi kupata huduma bora kwa gharama nafuu. Sisi kama wahariri tumeona ni muhimu kuunga mkono juhudi hizi kwa kuchangia ili kuwasaidia wale wasiokuwa na uwezo wa kumudu gharama za matibabu,” amessema Balile.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa BMH, Dkt. Abdalla Baja, amesema hospitali hiyo imeendelea kupanua wigo wa huduma za kibingwa na ubingwa bobezi, ikiwa na madaktari bingwa bobezi 18 pamoja na madaktari bingwa 20 wanaotoa huduma mbalimbali za matibabu ya hali ya juu.

Amesema mbali na huduma za upandikizaji figo na uroto, hospitali hiyo imefikia hatua ya kutoa huduma za upandikizaji wa uume kwa wagonjwa wenye changamoto zinazohitaji tiba hiyo maalumu.

Dkt. Baja aliongeza kuwa BMH imeandika historia kwa kuwa hospitali ya kwanza Afrika Mashariki kufanya upandikizaji wa uroto (selimundu), hatua ambayo imeifanya kuwa kituo muhimu cha rufaa kwa wagonjwa kutoka nchi mbalimbali za Afrika Mashariki na Kati.

Naye Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Damu, Dkt. Happiness Joseph Igogo, alisema hospitali hiyo imejipanga kuongeza idadi ya wagonjwa wanaopatiwa huduma za upandikizaji wa uroto kutoka wagonjwa 10 hadi 20 kwa mwaka.

Amesema mafanikio ya huduma hiyo yamechangia kwa kiasi kikubwa kupunguza vifo vinavyotokana na ugonjwa wa selimundu na kutoa matumaini mapya kwa wagonjwa wengi.

Kwa upande wake, Meneja wa Mkoa wa Dodoma wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF), Irene Kataraihya, alisema taasisi hiyo imejipanga kushiriki kikamilifu katika mfuko maalumu wa kusaidia huduma hizo muhimu ili kuendelea kuokoa maisha ya Watanzania.

Akizungumzia huduma za figo, Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Ndani na Figo, Dk. Ayubu Masamba, amesema huduma za upandikizaji figo zinazotolewa BMH zimepunguza kwa kiwango kikubwa idadi ya wagonjwa waliokuwa wakisafiri nje ya nchi kutafuta matibabu hayo.

Amesema hatua hiyo imechangia kupunguza gharama kubwa za matibabu kwa wagonjwa na familia zao huku ikiimarisha upatikanaji wa huduma za kibingwa ndani ya Tanzania.

Maadhimisho ya miaka 10 ya Hospitali ya Benjamin Mkapa yanatarajiwa kuwa fursa ya kuonesha mafanikio makubwa yaliyopatikana katika utoaji wa huduma za afya za kibingwa na ubingwa bobezi, huku hospitali hiyo ikiendelea kuwa kinara wa huduma za kisasa za matibabu nchini na katika ukanda wa Afrika Mashariki.



-Lumbila Wapata Umeme kwa Mara ya Kwanza Tangu Uhuru

-Giza la Miaka 60 Lamalizika Wilayani Ludewa


Ludewa, Njombe📍

Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kwa kushirikiana na mkandarasi; Shirika la Uzalishaji Mali JKT (SUMA JKT) leo, tarehe 25 Juni, 2026 kwa mara ya kwanza wamewasha umeme katika kitongoji cha Lumbila katika Halmashauri ya wilaya ya Ludewa ambapo eneo hilo lilikuwa halijapa umeme tangu Tanzania ipate uhuru wake 9 Desemba, mwaka 1961.

Akiongoza hafla hiyo ya kuwasha umeme kwa mara ya kwanza, Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB); Bodi inayoisimamia REA; Mhe. Balozi na Meja Jenerali Mstaafu, Jacob Kingu alisema utekelezaji wa mradi huo ni ushahidi wa dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha huduma ya umeme inawafikia Watanzania wote bila kujali umbali na changamoto za kijiografia.

Eneo hili lilikuwa halijawahi kupata umeme kwa zaidi ya miaka 60 tangu Tanzania ipate uhuru wake mwaka 1961. Hafla hiyo ya kuwasha umeme kwa mara ya kwanza katika Kitongoji cha Lumbila imefanyika katika Kanisa Katoliki la Kitongoji cha Lumbila, hatua iliyopokelewa kwa furaha kubwa na Wananchi wa eneo hilo.

Awali kabla ya kumkaribisha Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB); Mheshimiwa Balozi na Meja Jenerali Mstaafu, Jacob Kingu, Mhandisi, Thomas Mmbaga amaye alimwakilisha Mkurugenzi wa Umeme Vijijini alisema, Mradi wa kusambaza umeme kwenye vitongoji sita vya mwambao wa Ziwa Nyasa umetumia gharama ya Shilingi bilioni 3.124 na kuongeza kuwa hadi sasa mradi umefikia asilimia 67, ambapo vitongoji 3 kati ya 6 vya mwambao wa Ziwa Nyasa vimeshawashiwa umeme.

Mhandisi Mmbaga ameongeza kuwa Mradi unahusisha ujenzi wa kilomita 36.6 za njia za msongo wa kati na kilomita 15.1 za msongo mdogo.

“Mradi unatarajiwa kuwafikia wateja 151 wa njia moja (single-phase) na wateja 9 wa njia tatu (three-phase). Tayari kaya zaidi ya 23 zimeomba kuunganishiwa”. Amekaririwa, Mhandisi, Mmbaga.

Naye, Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya SUMA JKT Company Ltd, Meja James Simon Mwame, alisema utekelezaji wa Mradi huo ulikuwa na changamoto kubwa kutokana na mazingira ya mwambao wa Ziwa Nyasa, lakini juhudi za wataalam na wafanyakazi wa kampuni hiyo zimewezesha ndoto ya Wananchi kupata umeme kutimia.

Meja Mwame alisema SUMA JKT ni kampuni inayojihusisha na ujenzi na usambazaji wa miundombinu ya umeme nchini, na kwa Mkoa wa Njombe kampuni hiyo inatekeleza miradi ya usambazaji umeme katika wilaya za Ludewa na Makete.

Ziara ya viongozi (ikiongozwa na Mwenyekiti wa Bodi ya REA, Balozi Jacob Kingu) ilihusisha safari ya majini kwa boti ya takribani kilomita 11 kutoka Pwani ya Matema (Kyela, Mbeya) hadi Ludewa kutokana na ugumu wa kijiografia na miundombinu ya usafirishaji wa vifaa.

Mwananchi wa eneo hilo, Bakari Gowele, amebainisha kuwa umeme huo utasaidia sana sekta ya uvuvi kwani sasa wataweza kutengeneza barafu na kuhifadhi samaki kwa muda mrefu ili kuwafikisha kwenye masoko ya mbali wakiwa katika ubora wa hali ya juu.








-Asilimia 80 ya Mizigo Inaingia Tanzania Kwa Njia ya Maji

NA MWANDISHI WETU, KIGOMA

WAZIRI wa Uchukuzi, Profesa Makame Mnyaa Mbarawa, amesema mabaharia ni nguzo muhimu ya usafirishaji duniani na walinzi wakuu wa mnyororo wa biashara na uchumi, hivyo wanapaswa kuendelea kupewa mazingira bora ya kazi, mafunzo na fursa za maendeleo ili kuongeza mchango wao katika uchumi wa taifa.

Profesa Mbarawa ametoa kauli hiyo wakati wa kilele cha Maadhimisho ya 16  Siku ya Mabaharia Duniani yaliyofanyika mkoani Kigoma.

Alisema zaidi ya asilimia 80 ya biashara ya dunia husafirishwa kwa njia ya maji, jambo linalowafanya mabaharia kuwa mhimili muhimu wa uchumi wa kimataifa licha ya kukabiliwa na changamoto mbalimbali wanazokutana nazo ikiwemo kukaa muda mrefu baharini, kutengana na familia zao, mazingira magumu ya kazi na hatari za kiusalama, bado wanaendelea kutekeleza majukumu yao kwa weledi na kujitolea.

“Mabaharia ndio uti wa mgongo wa sekta ya usafirishaji duniani. Kazi yao inahakikisha bidhaa muhimu zinafika kwa wakati na uchumi wa dunia unaendelea kuzunguka. Tunawapongeza kwa moyo wao wa kujitolea na uzalendo,” alisema.

Amesema kauli mbiu ya maadhimisho hayo inapaswa kutekelezwa kwa vitendo kupitia sera madhubuti, utoaji wa mafunzo ya kisasa na kuimarisha ushirikiano wa kimataifa ili kuhakikisha sekta ya usafiri majini inakua sambamba na mahitaji ya dunia ya sasa.

“Mabaharia ni mhimili mkubwa wa uchumi wa dunia. Tunapaswa kuhakikisha wanapatiwa mafunzo yanayoendana na mabadiliko ya teknolojia na mazingira ya kazi ili waweze kukabiliana na kasi ya mabadiliko yanayotokea duniani,” amesema Profesa Mbarawa.

Ameeleza kuwa maadhimisho ya mwaka huu yanaenda sambamba na juhudi za Serikali za kuongeza uwekezaji katika shughuli za usafirishaji na uchumi wa bluu, hatua ambayo imeendelea kufungua fursa nyingi za ajira kwa vijana na wanawake.

Kwa mujibu wa Waziri huyo, ongezeko la ajira katika sekta ya usafiri majini linaendana na malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayolenga kukuza uchumi, kuongeza uzalishaji na kuboresha maisha ya wananchi.

Aidha, amesema Tanzania na Uganda zimeingia katika makubaliano ya ushirikiano wa shughuli za utafutaji na uokoaji majini, huku akieleza kuwa utekelezaji wa sheria na mifumo ya utafutaji na uokoaji utasaidia kuimarisha usalama wa mabaharia, abiria na vyombo vya usafiri majini.

Profesa Mbarawa amewataka mabaharia kuendelea kuwa waadilifu, kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za kazi pamoja na kutoa taarifa kwa mamlaka husika pindi wanapobaini changamoto zinazoweza kuhatarisha usalama wa vyombo na watu.

Amesema maadhimisho hayo yamekuwa jukwaa muhimu la utoaji elimu, kubadilishana uzoefu na kutoa maelekezo yatakayosaidia kukuza sekta ya usafiri wa majini nchini.

Katika hatua nyingine, ameliagiza Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC) kuharakisha utekelezaji wa mikakati ya kuwatafutia mabaharia wa Tanzania fursa zaidi za ajira katika soko la kimataifa, huku akisisitiza umuhimu wa kuwapa wanawake kipaumbele katika ajira za sekta hiyo.

Pia ameitaka TASAC kukamilisha kanzidata ya mabaharia nchini pamoja na kufanya tathmini ya mifumo ya maslahi yao ili kuhakikisha ustawi wa mabaharia unaimarishwa na changamoto zao zinapatiwa ufumbuzi kwa wakati.

Vilevile, ameshauri TASAC kuendelea kufanya mazungumzo na wamiliki wa meli mbalimbali ili waweze kufungua ofisi zao nchini Tanzania hatua itakayorahisisha upatikanaji wa ajira kwa mabaharia wa Kitanzania na kuongeza ushindani wao katika soko la kimataifa.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa TASAC Mohamed Salum amesema kuwa TASAC imesaini mikataba mbalimbali ya Kimataifa hatua ambayo itasaidia kuongeza uwigo wa ajira kwa mabaharia.

Amesema kuwa Serikali imefanya uwekazaji katika bandari ambapo fursa zimeongezeka kwa mabaharia pamoja kuendelea kuratibu katika mfumo kwa mabaharia kuwa kwenye mfumo huo.

Aidha amesongeza kuwa TASAC imenunua Boti za uokozi ili kuhakikisha wananchi na mabaharia wanakuwa salama wakati wote na wakipata majanga wanaokolewa.

Waziri wa Uchukuzi Profesa Makame Mnyaa Mbarawa (MB)akifunga maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani   yaliyofanyika Viwanja vya Center mjini Kigoma
Mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa ,Mkuu wa Wilaya ya Kigoma Dkt.Rashid Chuachua akizungumza wakati wa kumkaribisha mgeni rasmi katika Kilele cha maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani   yaliyofanyika Viwanja vya Center mjini Kigoma.
Mwenyekiti wa Bodi ya TASAC Nah.Mussa Mandia akitoa maelezo katika kilele cha  maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani   yaliyofanyika Viwanja vya Center mjini Kigoma.
Mkurugenzi Mkuu wa TASAC Mohamed Salum akitoa maelezo kuhusiana na umhimu wa mabaharia  katika maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani   yaliyofanyika Viwanja vya Center mjini Kigoma.
Mkuu wa Chuo cha DMI Profesa Tumain Gurumo akizungumza katika kilele cha maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani   yaliyofanyika Viwanja vya Center mjini Kigoma.


Picha za makundi mbalimbali katika kilele katika maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani   yaliyofanyika Viwanja vya Center mjini Kigoma.


Timu ya wataalamu kutoka Ofisi ya Rais–UTUMISHI kwa kushirikiana na Watumishi Housing Investment imefanya ziara ya ukaguzi wa miradi ya ujenzi wa nyumba za watumishi awamu ya pili katika Wilaya ya Dodoma, ikiwa ni sehemu ya kuhakikisha miradi hiyo inatekelezwa kwa kuzingatia ubora, thamani ya fedha na ratiba iliyopangwa.

Ziara hiyo imeongozwa na Mkurugenzi wa Kitengo cha Ufuatiliaji na Tathmini, Bw. Patrick Allute, ambaye amesema Serikali imeendelea kuimarisha mazingira ya kazi na makazi ya watumishi wa umma ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma kwa wananchi.

Bw. Allute amesisitiza umuhimu wa usimamizi madhubuti wa miradi, matumizi sahihi ya rasilimali za umma na ukamilishaji wa kazi kwa wakati huku viwango vya ubora vikizingatiwa. Aidha, ametoa maelekezo kwa wasimamizi wa miradi na wakandarasi kushughulikia kwa haraka changamoto zilizobainika ili kuhakikisha malengo ya miradi hiyo yanafikiwa kama ilivyopangwa.

Ziara hiyo imekuwa sehemu ya juhudi za Serikali za kuimarisha ufuatiliaji wa miradi ya maendeleo ili kuhakikisha uwekezaji unaofanywa unaleta matokeo yaliyokusudiwa kwa manufaa ya watumishi wa umma na wananchi kwa ujumla.

Katika ukaguzi huo, timu imetembelea miradi ya ujenzi wa nyumba za watumishi katika Kituo cha Afya Hombolo, Shule ya Sekondari Mtemichiloloma, Kituo cha Afya Mkonze na Shule ya Sekondari Bihawana, ambapo imejionea maendeleo ya utekelezaji wa miradi hiyo na imefanya majadiliano na wasimamizi pamoja na wakandarasi kuhusu hatua zilizofikiwa na changamoto zinazojitokeza.




Top News