Benki ya NMB imesisitiza umuhimu wa kupeleka elimu ya fedha kwa umma sambamba na kupanua huduma rasmi za kifedha, ikisema ujumuishaji wa kifedha unahitaji vijana kuelewa kuweka akiba, kupanga matumizi, kutumia huduma za kidijitali kwa usalama na kukopa kwa uwajibikaji.

Akizungumza katika Tamasha la Twen’Zetu kwa Yesu 2026 katika Viwanja vya Tanganyika Packers, Kawe, Dar es Salaam, Afisa Mkuu wa Wateja Binafsi na Biashara wa NMB, Filbert Mponzi, alisema vijana wanapaswa kujifunza kusimamia fedha zao mapema na kutumia teknolojia pamoja na vipaji vyao kujenga vyanzo vya kipato.

Katika tamasha hilo, NMB ilitoa elimu kuhusu akiba, mikopo, bima na huduma za kidijitali. Tawi Linalotembea la NMB—Bank on Wheels—pamoja na mawakala wa benki hiyo pia walitoa huduma za kifedha, zikiwemo kufungua akaunti na kufanya miamala.

Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Askofu Dkt. Alex Gehaz Malasusa, aliwataka vijana kuunganisha fursa za kiuchumi na maadili, huku mshiriki Jennifer Minja akisema mafunzo hayo yameongeza uelewa wake kuhusu umuhimu wa akaunti, akiba na matumizi yanayowajibika ya mikopo.

Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Askofu Dk. Alex Malasusa (kushoto), akizungumza na Afisa Mkuu wa Wateja Binafsi na Biashara wa NMB Bank Plc, Filbert Mponzi (wa pili kulia), na Mkuu wa Mauzo na Mtandao wa Matawi wa NMB, Donatus Richard (wa pili kushoto), mara baada ya kuzindua rasmi Tamasha la Twen’Zetu kwa Yesu katika Viwanja vya Tanganyika Packers, Kawe, Dar es Salaam. Kulia ni Mkurugenzi Mtendaji wa Upendo Media, Neng’ida Johanes. NMB ilikuwa mdhamini mkuu wa tamasha hilo.











Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali itaendelea kulinda uhuru wa kuabudu na kuimarisha ushirikiano na taasisi za dini kwa kutambua mchango mkubwa unaotolewa na taasisi hizo katika kujenga maadili, amani, mshikamano na maendeleo ya Taifa.

Dkt. Mwigulu amesema hayo leo, Jumapili Juni 14, 2026, aliposhiriki Ibada katika Kanisa la Tanzania Assemblies of God (TAG) Kiomboi Christian Centre, mjini Kiomboi, Wilaya ya Iramba mkoani Singida.

Ibada hiyo iliongozwa na Askofu wa Jimbo la Singida Kaskazini, Dkt. Danford Obadia pamoja na Mchungaji Kiongozi wa Kanisa hilo, Yona Suleman Essya.

Akizungumza na waumini hao, Waziri Mkuu amesema Serikali inatambua nafasi muhimu ya taasisi za dini katika malezi ya jamii na kwamba itaendelea kuweka mazingira rafiki yatakayowezesha taasisi hizo kutekeleza majukumu yake kwa uhuru na ufanisi.

“Sisi wote tutaendelea kulinda mazingira bora ya kuendesha ibada. Serikali itaendelea kutambua na kuamini kazi inayofanywa na taasisi za dini katika kujenga Taifa letu,” amesema Dkt. Mwigulu.

Amesema taasisi za dini zimekuwa mshirika muhimu wa Serikali katika kujenga maadili mema, kuhimiza uwajibikaji, kuimarisha mshikamano wa kijamii na kupambana na vitendo vinavyokinzana na utu na maendeleo ya wananchi.

Waziri Mkuu amesema Kanisa la TAG limekuwa na mchango mkubwa katika kuelimisha jamii, kuondoa imani potofu na kuhamasisha wananchi kuzingatia maadili na misingi sahihi ya maisha.

“TAG haikusimama kwenye ibada pekee, bali imebadilisha hata maisha ya kila siku ya wananchi. Imechangia kuondoa baadhi ya mila na imani zilizokuwa zinarudisha nyuma maendeleo ya watu wetu,” amesema.

Wakati huo huo, Dkt. Mwigulu ametoa rai kwa wananchi kuendelea kuheshimu nyumba za ibada na kuepuka kuziingiza katika shughuli zinazoweza kuvuruga dhamira na malengo yake ya msingi.

“Ukitaka siasa anzisha chama cha siasa. Usipeleke fujo kwenye nyumba ya ibada. Lazima tuendelee kuheshimu utakatifu wa nyumba zetu za ibada,” amesema.

Aidha, Waziri Mkuu amesema Serikali itaendelea kupokea ushauri na maoni kutoka kwa viongozi wa dini ili kuboresha zaidi mazingira ya utoaji huduma kwa wananchi na kuimarisha maendeleo ya Taifa.

Awali akimkaribisha Waziri Mkuu kuzungumza na waumini, Askofu wa Jimbo la Singida Kaskazini, Dkt. Danford Obadia amesema kanisa linaendelea kumuombea Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na viongozi wa Serikali ili waendelee kutekeleza majukumu yao kwa hekima, uadilifu na mafanikio kwa manufaa ya Taifa.

Askofu Obadia amesema Watanzania wana wajibu wa kuliombea Taifa na viongozi wake kwa mujibu wa mafundisho ya Biblia ili nchi iendelee kudumisha amani, utulivu na maendeleo.

“Kabla ya mambo yote, nataka dua na sala na maombezi yafanyike kwa ajili ya wafalme na wenye mamlaka, ili tuweze kuishi kwa amani na utulivu. Hii nchi ni ya kwetu; tukiipenda nchi yetu na kuwaombea viongozi wetu, tutakaa nchi hii salama na tutaondoka duniani salama,” amesema Askofu Obadia.






WITO umetolewa kwa wanawake nchini kuchangamkia fursa za uwekezaji katika mifuko mbalimbali ya uwekezaji, Ili kufikia Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 na kuliwezesha Taifa kuwa na uchumi shirikishi wa viwanda unaowezeshwa na ushirikishwaji mpana wa huduma za kifedha.

Wito huo umetolewa na Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Dar es Salaam na Mwenyekiti wa Kikundi cha Wanawake cha Huduma ndogo za kifedha cha Diamond Divas, Mhe. Janeth Elias Mahawanga wakati wa semina kuhusu Uwekezaji wa wanawake katika mifuko ya uwekezaji akisema uwekezaji huo utawasaidia kuongeza Mitaji ya biashara zao hivyo kujiinua kiuchumi.

“Tunapozungumzia Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 kwa upande wa wanawake, Dira inasema Uchumi wa wananchi mmoja mmoja unakwenda kuongezeka, na Uchumi wa Taifa, lakini pia viwanda vidogo vidogo, Rais Samia Suluhu Hassan alikuwa na maono ya kuwa na dira ya Taifa, utekeleza wa dira unatutegemea sisi wananchi, sisi wanawake tunataka kuingia moja kwa moja katika utekelezaji wa dira, tunataka kuingia katika uchumi wa viwanda tukawe wawekezaji katika Taifa letu.

“Kupitia semina kama hizi, ili kuwaandaa wanawake kushiriki kikamiifu, ni lazima kuwajengea uwezo kufahamu elimu ya fedha, biashara, fursa mbalimbali na uwekezaji, na ndio maana kwenye elimu hii sisi kama kikundi cha Diamond Divas tunataka kuwa wawekezaji, tunataka kuanzisha viwanda, tuanzishe taasisi yetu ndogo ya fedha, ili tuweze kuyafanya yote haya lazima tujikite zaidi katika elimu ya fedha, biashara, fursa na uwekezaji,”alisema Mhe Janeth.

Akizungumzia nini kifanyike Ili kuongeza kasi ya watanzania hususan wanawake kuwekeza katika mifuko ya uwekezaji na Masoko ya mitaji, Mkufunzi wa Masuala ya kifedha, uchumi na uwekezaji, Bw. Emilian Busara alitaja suala la utoaji wa elimu kuhusu mifuko hiyo kupewa kipaumbele zaidi Ili wanaotaka kuwekeza wachague ni aina gani ya mfuko unawafaa.

“Cha kwanza watanzania wanahitaji elimu ya fedha, bila kuwapa watu elimu, hakuna namna nyingine ambayo watu wanaweza kuijua mifuko ya uwekezaji, jinsi ya kuwekeza na manufaa yake, na la pili ni kuchukua hatua ya kuwekeza, huwezi kujifunza kuendesha baisketi kwa kusoma kwenye vitabu, lakini tatu ni yule anayejua basi amuelimisha mwingine, yakifanyika haya, sina shaka idadi ya watanzania hususan wanawake watakaojiunga na mifuko hii itaongezeka,” alisema Bw. Busara akitoa pongezi kwa kikundi cha Diamond Divas kwa kuonesha njia.

Kwa upande wake, mmoja wa washiriki katika semina hiyo, Bi. Hellen Siria alitoa ushauri kwa wanawake walio katika vikundi vya kuwezeshana katika Jamii kuvirasimisha Ili viweze kunufaika na fursa mbalimbali zinazotolewa ikiwemo fursa za kupata mitaji, mikopo ya aina mbalimbali na fursa nyinginezo zitakazowasaidia kuinua biashara na maisha yao.

“Wito wangu kwa wanawake wenzangu, hasa kwenye vile vikundi vilivyopo katika jamii, tuvirasimishe ili iwe rahisi kunufaika na fursa mbalimbali zinazojitokeza zinazowahusu wanawake wajasiriamali, lakini kilicho muhimu zaidi kwa wanawake tuhakikishe tunajikita katika uwekezaji,” alisema Bi. Hellen.


Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Dar es Salaam na Mwenyekiti wa Kikundi cha Vicoba cha Diamond Divas Group, Mhe. Janeth Elias Mahawanga, akizungumza katika semina iliyoandaliwa na kikundi hicho ikihusu elimu ya kifedha na jinsi ya kuwekeza katika mifuko ya uwekezaji iliyofanyika jijini Dar es Salaam jana.



Katibu wa Kikundi cha Vicoba cha Diamond Divas Group, Bi.Noryne Mmasi, akizungumza katika semina iliyoandaliwa na kikundi hicho ikihusu elimu ya kifedha na jinsi ya kuwekeza katika mifuko ya uwekezaji iliyofanyika jijini Dar es Salaam jana.


Mkufunzi wa Masuala ya kifedha, uchumi na uwekezaji, Bw. Emilian Busara, akitoa elimu ya fedha na uwekezaji katika semina iliyoandaliwa na Kikundi cha Vicoba cha Diamond Divas Group ikihusu elimu ya kifedha na uwekezaji iliyofanyika jijini Dar es Salaam jana.


Baadhi ya wanachama wa Kikundi cha Vicoba cha Diamond Divas Group wakisikiliza mada iliyokuwa ikitolewa na Mkufunzi wa Masuala ya kifedha, uchumi na uwekezaji, Bw. Emilian Busara katika semina kuhusu elimu ya kifedha na jinsi ya kuwekeza katika mifuko mbalimbali ya uwekezaji, iliyofanyika jijini Dar es Salaam jana.


Wanachama wa Kikundi cha Vicoba cha Diamond Divas Group, wakipozi mbele ya wapigapicha mara baada ya kumalizika kwa semina iliyoandaliwa na kikundi hicho kuhusu elimu ya kifedha na jinsi ya kuwekeza katika mifuko mbalimbali ya uwekezaji, iliyofanyika jijini Dar es Salaam jana.



Na. Jawadu Kinyobwa – Mtwara

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Jakaya Kikwete (Mb), amewataka wahitimu wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) kutumia maarifa, ujuzi na stadi walizopata chuoni kuchangia maendeleo ya Taifa na kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Akizungumza wakati wa Mahafali ya 43 ya Chuo TPSC Kampasi ya Mtwara, yaliyofanyika Juni 13, 2026, Mhe. Kikwete amewapongeza wahitimu 1,926 waliohitimu katika ngazi ya Astashahada, Stashahada na Shahada ya Kwanza kwa juhudi, nidhamu na uvumilivu uliowawezesha kufikia mafanikio hayo.

Alisema kuwa kuhitimu masomo si mwisho wa kujifunza bali ni mwanzo wa safari mpya ya kuitumikia jamii na Taifa, huku akiwataka wahitimu kuwa mabalozi wazuri wa Chuo kwa kuzingatia maadili, uwajibikaji, uzalendo na ubunifu katika maeneo yao ya kazi na maisha ya kila siku.

“Taifa linahitaji wataalamu wenye uwezo wa kutatua changamoto, kuleta ubunifu na kuongeza tija katika sekta za umma na binafsi. Maarifa mliyoyapata yanapaswa kutafsiriwa katika matendo yenye manufaa kwa jamii na Taifa kwa ujumla,” alisema Mhe. Kikwete.

Aidha, Waziri Kikwete alisema Tanzania inaelekea katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 ambayo inahitaji wataalamu wenye maarifa na umahiri wa kutekeleza maeneo mbalimbali ya kimkakati. Alieleza matumaini yake kuwa wahitimu hao watakuwa sehemu ya nguvu kazi itakayochangia kufikiwa kwa malengo ya dira hiyo.

Katika hatua nyingine, Mhe. Kikwete alipongeza Chuo kwa kuendelea kuimarisha matumizi ya teknolojia katika utoaji wa mafunzo kupitia mifumo ya mtandaoni, hatua ambayo imeongeza upatikanaji wa elimu kwa makundi mbalimbali ndani na nje ya nchi.

Alisisitiza kuwa Serikali itaendelea kuhamasisha matumizi ya teknolojia za kisasa katika taasisi zake ili kuongeza ufanisi, kupunguza gharama za utoaji huduma na kupanua wigo wa huduma kwa wananchi.

Kuhusu tafiti, Waziri Kikwete alisema Serikali inatambua umuhimu wa tafiti zenye ubora katika kutoa suluhisho la changamoto za maendeleo na kusaidia kufanya maamuzi yanayotokana na ushahidi. Hivyo, aliitaka Menejimenti ya Chuo kuendelea kuimarisha shughuli za utafiti ili ziwe na mchango mkubwa zaidi katika maboresho ya sera, mifumo na huduma za umma.

Pia alipongeza juhudi za Chuo katika kuimarisha ushirikiano na taasisi mbalimbali za ndani na nje ya nchi, akitaja ushirikiano na Kenya School of Government pamoja na National School of Government ya Afrika Kusini kuwa sehemu ya hatua zinazochangia kuboresha ubora wa mafunzo na kuongeza hadhi ya taasisi hiyo.

Aidha, alitoa wito kwa waajiri wote wa umma kuhakikisha watumishi wapya wanapelekwa kwenye Mafunzo Elekezi ya Awali kwa mujibu wa taratibu za Serikali ili kuwajengea uelewa wa maadili, misingi, kanuni na utamaduni wa utumishi wa umma.

Akihitimisha hotuba yake, Mhe. Kikwete aliwataka wahitimu kutumia elimu waliyoipata kuleta mabadiliko chanya katika jamii, kuwa wachapakazi, wazalendo na waadilifu, huku akiwapongeza wahitimu, uongozi wa Chuo, wahadhiri, watumishi, wazazi na walezi kwa kufanikisha Mahafali ya 43 ya Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania.


Awali akitoa salaam za pongezi, Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais – Utumishi wa Umma na Utawala Bora Bw. Xavier Daudi Awali, amevitaka vyuo vya elimu ya juu kuhakikisha vinaandaa wahitimu wenye maarifa, ujuzi na umahiri unaokidhi mahitaji ya soko la ajira, ili waweze kushindana na kuchangia ipasavyo maendeleo ya Taifa.

Kwa upande wake, Mkuu wa Chuo na Mtendaji Mkuu wa Chuo hicho, Dkt. Ernest Mabonesho amesema mazingira ya sasa ya utumishi wa umma yanahitaji matumizi ya teknolojia za kidijitali, akili bandia (AI) na mifumo ya maamuzi inayozingatia ushahidi wa kisayansi ili kuongeza ufanisi, uwajibikaji na ubora wa huduma zinazotolewa kwa wananchi.

"Kutokana na mabadiliko hayo, Chuo kimeendelea kuboresha mifumo ya ufundishaji na ujifunzaji kwa kutumia teknolojia za kisasa, kwa lengo la kuzalisha wahitimu wenye maarifa, ujuzi na stadi zinazowawezesha kuajiriwa, kujiajiri na kutoa mchango chanya katika maendeleo ya Taifa kupitia soko la ajira la ndani na kimataifa."Kuzingatia maadili ya umma baada ya kumaliza.












KATIKA kuadhimisha Siku ya Mazingira Duniani, wafanyakazi wa Benki ya Absa kwa kushirikina Shirika la Uhifadhi wa Mazingira (WWF), wamepanda miti 1300  katika Msitu wa Pugu Kazimzumbwi, Wilayani Kisarawe, mkoani Pwani mwishoni mwa wiki huku benki hiyo ikiahidi kuyafanya matukio hayo kuwa endelevu.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi wa Masoko na Mawasiliano wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Aron Luhanga alisema suala la upandaji miti ni jambo muhimu sana katika suala zima la uhifadhi wa mazingira kutokana na faida mbalimbali zinazotokana na misitu.    

“Benki ya Absa lengo lake kuu linasema ‘Kuiwezesha Afrika ya Kesho, Pamoja, Hatua Moja Baada ya Nyingine’, kwa kupanda miti katika eneo hili la Pugu Kazimzumbwi, tunaamini tunasaidia kuwawezesha wakazi wa Dar es Salaam kuwa na afya njema inayotokana na hewa safi kutoka mahali hapa kwani Kazimzumbwi ndio mapafu yanayolifanya jiji la Dar es salaam lipumue kwa kufyonza hewa chafu inayotoka humo.

“Absa pia tunasema, Stori yako ina Thamani’ tunaamini kila stori ya mtanzania ina thamani sana kwetu, hivyo kwa kuja kupanda miti tukishirikiana na Shirika la WWF, tunaamini tumekuja kuandika Stori ya Jiji la Dar es salaam kwa kuhakikisha kwamba miti hii tunayopanda inawezesha utoaji wa hewa safi, kuleta chanzo cha mvua na kuleta mandhari nzuri na kuwa sehemu nzuri ya kutembelea,” alisema Bw. Luhanga.

 Naye Mkuu wa Kitengo cha Fedha na Utawala wa Shirika la Uhifadhi wa Mazingira (WWF), Bw. Manyerere Wajama, akimwakilisha mkurugenzi wa shirika hilo katika hafla hiyo alisema kwa kushirikia na Benki ya Absa tukio ni uwekezaji mkubwa katika suala la hewa safi na utunzaji wa mazingira, na pia msitu huo ni rasilimali kubwa kwa wakazi wa Kisarawe,  kwenye hewa safi kwa sababu msitu unanyonya hewa chafu, kwenye ecology ya mazingira na pia msitu wa Pugu Kazimzumbwi  ni muhimu kwenye kusaidia shughuli za wananchi wa eneo la kisarawe na maeneo Jirani.

“Kwa kupanda miti tunawekeza katika maisha ya baadae ya watoto wetu, kwa sababu kwa kuhifadhi mazinigira leo tunategemea watu wataendelea kuishi kwenye mazingira safi na salama, tunahitaji ushirikiano, serikali, sekta binafsi pamoja na wakazi wa eneo hili, leo tukiondoka mwanajamii akaingiza mifugo yake maeneo haya tunakuwa hatujafanya kitu chochote,  kwahiyo ili kazi yetu iwe na maana tunatakiwa tushirikiane,” alisema Bw. Wajama akitoa shukurani kubwa kwa Benki ya Absa kwa kuwa wadau wao muhimu katika suala la uhifadhi wa mazingira.

Awali Naibu Ofisa Misitu wa Wilaya ya Kisarawe, Bw. Idd Mbaruku alisema zoezi la upandaji wa miti 1300 kutoka Benki ya Absa wakishikiana na WWF ni muendelezo wa jitihada ya utunzaji wa mazingira hasa katika hifadhi yao ya Pugu Kazimzumbwi huku wakishirikiana karibu na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS).

“Kama inavyoelezwa msitu huu ndio mapafu ya jiji letu la Dar es Saalam, lakini pia ndio mbavu za wilaya yetu ya Kisarawe kutokana na umuhimu wake kwa sababu hapa tupo karibu sana na Dar es salaam na kama tunavyojua jiji hilo lina viwanda vingi, kuna mchafuko mkubwa wa hali ya hewa, kwahiyo msitu huu umekuwa ni sehemu ya kufyonza hiyo hewa chafu, kwa hiyo sisi kama serikali kwa kushirikiana na jamii inayotuzunguuka tutahakikisha miti hii iliyopandwa inazidi kukua,” alisema Bw. Mbaruku.

Mkurugenzi wa Masoko na Mawasiliano wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Aron Luhanga (kushoto), Mkurugenzi wa Kitengo cha Huduma kwa Wateja na Huduma za Kidigitali wa Benki ya Absa Tanzania, Samuel Mkuyu ( katikati ), na Mhifadhi Misitu wa Wilaya ya Kisarawe, Bw. Baraka Mtewa wakishirikiana kupanda miti kama sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Mazingira duniani, kwa kushirikiana na Shirika la Uhifadhi wa Mazingira (WWF), katika msitu wa Pugu Kazimzumbwi, Wilayani Kisarawe, mkoani Pwani jana. Benki ya Absa imepanda miti 1300 ikishirikiana na shirika hilo.

Mkurugenzi wa Masoko na Mawasiliano wa benki hiyo, Bw. Aron Luhanga (kushoto), na Mkurugenzi wa Kitengo cha Huduma kwa Wateja na Huduma za Kidigitali wa Benki ya Absa Tanzania, Samuel Mkuyu, wakipanda miti kama sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Mazingira duniani, kwa kushirikiana na Shirika la Uhifadhi wa Mazingira (WWF), katika msitu wa Pugu Kazimzumbwi, Wilayani Kisarawe, mkoani Pwani jana. Benki ya Absa imepanda miti 1300 ikishirikiana na Shirika la WWF.

Meneja Huduma za Jamii na Matukio wa Benki ya Absa Tanzania, Bi. Abigail Lukuvi (kushoto) na Mkuu wa Kitengo cha Fedha na Utawala wa Shirika la Uhifadhi wa Mazingira (WWF), Bw. Manyerere Wajama, wakipanda miti kama sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Mazingira duniani, katika msitu wa Pugu Kazimzumbwi, Wilayani Kisarawe, mkoani Pwani jana. Benki ya Absa imepanda miti 1300 ikishirikiana na Shirika la WWF.

Meneja Huduma za Jamii na Matukio wa Benki ya Absa Tanzania, Bi. Abigail Lukuvi (kulia), Mhifadhi Misitu wa Wilaya ya Kisarawe, Bw. Baraka Mtewa na Mkuu wa Kitengo cha Fedha na Utawala wa Shirika la Uhifadhi wa Mazingira (WWF), Bw. Manyerere Wajama, wakishirikiana kupanda miti kama sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Mazingira duniani, katika msitu wa Pugu Kazimzumbwi, Wilayani Kisarawe, mkoani Pwani jana. Benki ya Absa imepanda miti 1300 ikishirikiana na Shirika la WWF.
Baadhi ya wafanyakazi wa Benki ya Absa Tanzania walipanda miti, kama sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Mazingira duniani, kwa kushirikiana na Shirika la Uhifadhi wa Mazingira (WWF), katika msitu wa Pugu Kazimzumbwi, Wilayani Kisarawe, mkoani Pwani jana. Benki ya Absa imepanda miti 1300 ikishirikiana na shirika hilo.
Wafanyakazi na viongozi wa Benki ya Absa Tanzania, wawakilishi kutoka Shirika la Uhifadhi wa Mazingira (WWF), Viongozi wa Kiserikali kutoka Wilaya ya Kisarawe, wawakilishi kutoka Ofisi ya Misitu wilaya, Wakala wa Misitu (TFS), na wadau wengine wa mazingira wakipozi kwa picha ya kumbukumbu muda mfupi baada ya kukamilika kwa zoezi la upandaji miti katika Msitu wa Pugu Kazimzumbwi, Wilayani Kisarawe, Mkoani Pwani jana, kama sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani.  
Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali imewasilisha bungeni mapendekezo yatakayowezesha fedha za miradi ya maendeleo katika sekta za maji, barabara na nishati kupelekwa moja kwa moja kwenye mifuko husika ili kuongeza kasi ya utekelezaji wa miradi na kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.

Dkt. Mwigulu amesema hayo leo, Jumamosi Juni 13, 2026, alipokuwa akizungumza na wananchi wa Tarafa ya Ndago katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika Uwanja wa Shule ya Msingi Ndago, Wilaya ya Iramba mkoani Singida.

Amesema hatua hiyo inalenga kuhakikisha fedha zinazotengwa kwa ajili ya utekelezaji wa miradi zinafika moja kwa moja katika sekta husika na kuwezesha utekelezaji wa miradi kufanyika kwa ufanisi na kwa wakati.

“Fedha zote zinazokwenda kwenye barabara, maji na umeme hazitapita tena kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali. Zitakwenda moja kwa moja kwenye mifuko husika ili kuhakikisha utekelezaji wa miradi unaongezeka kasi,” amesema Dkt. Mwigulu.

Waziri Mkuu amesema hatua hiyo itaongeza kasi ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo ambayo utekelezaji wake ulipungua katika kipindi kilichopita kutokana na Serikali kuelekeza rasilimali nyingi katika kukamilisha miradi mikubwa ya kimkakati ya Taifa.

Ametaja baadhi ya miradi hiyo kuwa ni Mradi wa Kufua Umeme wa Julius Nyerere (JNHPP), Daraja la Kigongo–Busisi pamoja na Reli ya Kisasa (SGR), ambayo kwa sasa imekamilika au imefikia hatua kubwa za utekelezaji.

“Tulifanya uamuzi wa kimkakati na wa kizalendo wa kukamilisha miradi hiyo kwa sababu ilikuwa muhimu kwa mustakabali wa Taifa. Sasa miradi hiyo imekamilika au imefikia hatua kubwa za utekelezaji na hivyo kasi ya utekelezaji wa miradi mingine itaongezeka,” amesema.

Katika hatua nyingine, Dkt. Mwigulu amesema Serikali itaongeza kasi ya utekelezaji wa mradi wa Barabara ya Kizaga–Ndago–Sepuka–Singida, ambayo ni miongoni mwa miradi muhimu ya miundombinu inayounganisha maeneo makubwa ya uzalishaji wa mazao katika Wilaya ya Iramba.

Amesema Serikali inatambua umuhimu wa barabara hiyo katika kuchochea shughuli za uzalishaji, biashara na usafirishaji wa mazao hususan katika Tarafa za Ndago na Shelui ambazo ni miongoni mwa maeneo yanayoongoza kwa uzalishaji katika wilaya hiyo.

“Barabara hii ni muhimu sana kwa wananchi wetu. Ni barabara inayounganisha maeneo makubwa ya uzalishaji na ndiyo maana Serikali imeendelea kuipa kipaumbele katika mipango yake ya maendeleo,” amesema.

Aidha, Waziri Mkuu amesema Serikali itaendelea kutekeleza miradi ya madaraja katika maeneo mbalimbali ya Tarafa ya Ndago ili kuondoa changamoto za usafiri na usafirishaji, hususan katika maeneo yanayoathirika wakati wa mvua.

Amesema katika mwaka wa fedha unaoanza Julai 1, 2026, Serikali itaanza utekelezaji wa miradi mbalimbali ya madaraja pamoja na usanifu wa madaraja makubwa yatakayorahisisha mawasiliano na kuimarisha usalama wa wananchi.

Sambamba na hilo, Dkt. Mwigulu amesema Serikali inaendelea na hatua za kuendeleza kilimo cha umwagiliaji katika Bonde la Dengu kupitia usanifu wa miundombinu ya mabwawa na mifumo mingine ya kuhifadhi maji kwa ajili ya kuongeza tija katika uzalishaji wa mazao.

“Usanifu unaendelea katika Bonde la Dengu ili tuweze kuwa na miundombinu ya umwagiliaji itakayowezesha wananchi kuongeza uzalishaji na tija katika kilimo,” amesema.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amesema Serikali imeanza kutafuta suluhisho la kudumu la changamoto zinazowakabili wakulima katika mfumo wa stakabadhi ghalani kwa kuongeza uwekezaji katika ujenzi wa maghala kwenye maeneo ya uzalishaji.

Amesema hatua hiyo itapunguza gharama za usafirishaji wa mazao, kurahisisha uhifadhi wa mazao na kuongeza ufanisi wa utekelezaji wa mfumo wa stakabadhi ghalani.

“Tutajenga maghala katika maeneo ya uzalishaji wa mazao yanayotumia mfumo wa stakabadhi ghalani ili kupata suluhisho la kudumu la changamoto hii,” amesema.

Wakati huo huo, Dkt. Mwigulu ametangaza kupelekwa kwa gari jipya la wagonjwa (ambulance) katika Tarafa ya Ndago ndani ya wiki moja hadi mbili ili kuimarisha huduma za rufaa na dharura kwa wananchi wa eneo hilo.

Amesema ambulance hiyo itasaidia kuhudumia wananchi wa maeneo mbalimbali ya tarafa hiyo na kuongeza ufanisi wa utoaji wa huduma za afya.

“Ndani ya wiki moja hadi mbili ambulance mpya itakuwa imefika Ndago kwa ajili ya kuwahudumia wananchi wa tarafa hii,” amesema.










Na Victor Masangu, Kibaha

Madiwani wa chama cha mapinduzi (CCM) Mkoa wa Pwani wametakiwa kujenga mising imara iya kuwa na uzalendo na Taifa lao ikiwa pamoja na kuweka mikakati kabambe ya kupambana na kero na chanagamoto mbali mbali za wananchi ili kuweza kuzitafuta ufumbuzi.

Hayo yamebainishwa na Mjumbe wa halmashauri kuu ya (CCM) Taifa Mohamed Mchengerwa (MNEC) ambaye pia ni Waziri wa afya wakati wa kufungua mafunzo maalumu kwa madiwani wa CCM Mkoa wa Pwani ambayo yamefanyika katika shule ya uongozi ya Mwalimu Julias Nyerere iliyopo eneo la kwa mfipa katika Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha Mkoa wa Pwani.

Mchengerwa amesema kwamba mafunzo hayo kwa madiwani wa Mkoa wa Pwani watawajengea uwezo mkubwa katika suala zima la kuwatumikia wananchi wao ikiwemo kusikiliza kero na changamotto mbali mbali ambazo zinawakabili wanapaswa kuwa wazalendo.

Kadhalika Mchengerwa amesema kwamba madiwani wanapaswa kuabdilika na kuwa mstari wa mbele katika kwenda kuwa suluhisho katika kuwasikiliza wananchi na kushirikiana nao katika mambo mbali ya kijamii.

"Kwanza kabisa nipende kuchukua fursa hii kumpongeza kwa dhati kabisa Katibu wa chama caha mapinduzi (CCM) kwa kuweza kuwakutanisha kwa mara ya kwanza madiwani wote wa CCM wa Mkoa wa Pwani kwa hivyo kitu kikubwa ninachowaomba ni kuwa wazalendo na nchi yao na kuelekeza nguvu zao katika kutatua kero na changamoto za wananchi,"amebainisha Mchengerwa.

Pia Mchengerwa hakusita kugusia suala la madiwani hao kuwa na upendo, na mshikamano wa pamoja katika maeneo yao kwa lengo la kuweza kushirikiana bega kwa bega na wananchi kwa ajili ya kuweza kuwaletea maendeleo chanya.

Kwa uppande wake Katibu wa chama cha mapinduzi (CCM) Mkoa wa Pwani Ndg. Kiite Mfilinge amesema kwamba lengo kubwa la mafunzo hayo ni kuwakutanisha madiwani hao ili kuwajengea uwezo ikiwa pamoja na kuwakumbushia kutekeleza majukumu yao pamoja na kuwahudumia wananchi.

Katibu huyo amefafanya kwamba katika mafunzo hayo jumla ya madiwani wote wapatao 185 wameweza kupata fursa ya kushiriki na kwamba wamejifunzo mada mbali mbali ikiwemo suala la uzalendo, uwajibikaji, ulinzi na usalama ikiwa pamoja na kuwa na dira ya pamoja katika ngazi ya Mkoa ambayo itaweza kuleta matokeo ya namna bora ya kuwatumikia wannchi.

Kwa upande wake Mwalimu wa shule ya uongozi mwalimu Julias nyerere Profesa Mercellina Chijoriga ambaye pia alikuwa mtoa mada katika mafunzo hayo amesema amebainisha kuwa mafunzo hayo yataweza kuleta tija zaidi ya uwajibikaji katika suala zima la kuwahudumia wananchi katika maeneo yao.

Pia Profesa huyo ametumia mafunzo hayo kuwahimiza madiwani wa Mkoa wa Pwani kuzingatia kwa weledi na ufanisi mkubwa dira ya Taifa ambayo itaweza kuwasaidia kwa kiasi kikubwa kutimiza majukumu yao ipasavyo ikiwemo suala zima la utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Nao baadhi ya madiwani ambao wamehudhuria katika mafunzo hayo akiwemo Ally Simba Diwani wa Kata ya Misusugu pamoja na Diwani wa Kata ya Mwewe omary Msombwe wameahidi kwenda kuyatumia vema mafunzo hayo ambayo wameyapata na kwamba yameweza kuwajengea uwezo mkubwa katika kutekeleza majukumu yao.

Mafunzo hayo ya siku moja yamewajumuisha madiwani wote wa Mkoa wa Pwani waoatao 185 ambapo wamepata fursa ya kujifunz amada mbali mbali ikiwemo suala la uzalendo, ulinzi na amani, uwajibikaji kwa wananchi wao , jinsi ya kusimamia mapato, na kujifunza mambo mbali mbali amabyo yataweza kuwa ni mkombozi mkubwa katika maeneo yao.



MOSHI.

VIJANA wameaswa kutokukubali kurubuniwa, kushawishiwa wala kutumika kwa namna yoyote ili kuhatarisha Amani mshikamano na umoja wa Taifa kwa maslahi binafsi ya watu au makundi yenye nia zisizo njema kwa nchi.

Tamko hilo limetolewa leo na Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi mkoa wa Kilimanjaro, Ivan Moshi mara baada ya kumalizika kwa kikao cha Baraza la UVCCM mkoa wa Kilimanjaro kilichofanyika katika ukumbi wa CCM mkoa.

Akisoma tamko hilo, Moshi alisema kuwa, wanatambua athari kubwa zinazoweza kusababishwa na migogoro, vurugu na mipasuko ya kijamii katika Uchumi na ustawi wa wananchi na kutoa wito kwa vijana kuendelea kuzipuuza kauli, vitendo na propaganda zinazolenga kuleta taharuki, migawanyiko au kuvuruga amani.

“Baraza la UVCCM mkoa wa Kilimanjaro linawapongeza vijana wa Kilimanjaro na Tanzania kwa kuendelea kuonyesha uzalendo, uvumilivu, busara na mshikamano katika kuilinda amani na utulivu wa Taifa letu, tunatambua amani ndio msingi wa maendeleo ya kiuchumi, kijamii na kisiasa” alisema Ivan.






Top News