Na Karama Kenyunko Michuzi Tv 

MWANAMKE  Monica Beda (36), mkazi wa Kimara jijini Dar es Salaam amefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu akikabiliwa na shtaka la kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu kiasi cha shilingi milioni 60.

Katika hati ya mashtaka iliyosomwa mahakamani hapo leo Aprili 20,1026 na Wakili wa Serikali Cathbert Mbiling’i  imeileza mahakama kuwa mshtakiwa alitenda kosa hilo Novemba 8, 2025, katika Mtaa wa Samora, jijini Dar es Salaam.

Mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu Salome Mshasha, imedaiwa mshtakiwa alimlaghai Agrey Festo Mashanda kwa kujifanya angeweza kumuagizia gari aina ya Mitsubishi Fuso Fighter Damper lenye chassis namba  FK418F-550031, huku akijua kuwa si kweli.

Kwa mujibu wa upande wa mashtaka  upelelezi wa shauri hilo umekamilika na wameomba kupangiwa tarehe kwa ajili ya usikilizwaji wa awali (PH).

Hata hivyo mshtakiwa amekana kutenda kosa hilo na amerudishwa rumande kwa kushindwa kutimiza masharti ya dhamana 

Mahakama ilimpatia mshtakiwa dhamana kwa masharti ya kuwa na wadhamini wawili wa kuaminika, ambapo mmoja wao anatakiwa kuwasilisha hati ya mali isiyohamishika au fedha taslimu yenye thamani ya nusu ya fedha anazodaiwa kuiba, sawa na shilingi milioni 30.

Kesi hiyo limeahirishwa hadi Mei 6, 2026 kwa ajili ya mshtakiwa kusomewa maelezo ya awali.



Na Said Mwishehe,Michuzi TV

JUBILEE Health Insurance imetoa elimu kuhusu afya ya akili kwa wanafunzi wa Shule ya Sekondari Mzizima jijini Dar es Salaam lengo likiwa kuijengea uelewa jamii kuhusu afya ya akili huku ikieleza mpango huo utafanyika kwa wanafunzi wa shule mbalimbali nchini.

Akizungumza katika Shule ya Sekondari Mzizima jijini Dar es Salaam wakati wa kutolewa elimu kuhusu afya ya akili kwa wanafunzi 100 wa shule hiyo , Dk.Milembe Makoye ambaye ni Senior wellness officer kutoka Jubilee Health Insurance amesema wanaamini elimu ni ufunguo wa maisha hivyo wakielewa watajitambua.

“Tuko hapa kwa ajili ya kutoa elimu kuhusiana na afya ya akili lakini afya kwa ujumla.Kwanini tumeamua kutoa elimu hii ? Tunaamini wakielewa watajitambua.

“Kwanini afya ya akili ? Afya ya akili ni jambo ambalo ni changamoto kwa watu wengi sio kwa watu wazima pekee, lakini hata kwa watoto ambao wamekuwa wanasahaulika.

“Sasa kama Jubilee Health Insurance tunaamua kuingia kwenye jamii kuwagusa watoto wapate elimu sahihi waweze kujitambua ili hata wanapokua waweze kudhibiti changamoto ya matatizo ya afya ya akili lakini na afya ya mwili kwa ujumla,”amesema Dk.Makoye.

Aidha amesema Sekondari ya Mzizima ni ya kwanza kufikiwa lakini watakwenda shule nyingi zaidi kadri watakavyoweza huku akifafanua sababu za kuja na programu hiyo inatokana na ukweli Jubilee Health Insurance wanatoa huduma za bima ya afya.

“Lakini tukaona tusiishie kutoa tu bima basi tuguse jamii kwa kutoa elimu ya ustawi wa Afya, maana wakielewa maana ya afya ya akili watachukua njia sahihi ya kutunza afya zao na hapo tutakuwa tumefuzu.

Kwa upande wake Dkt.Isaac Marro akizungumza baada ya kutoa elimu ya afya ya akili kwa wanafunzi hao amesema kuna kila sababu ya Jamii kuwa na uelewa na afya ya akili mapema kwani kwa muda mrefu elimu kuhusu changamoto ya akili inatolewa kwa watu wazima.

“Kwa kifupi afya ya akili duniani kote imekuwa changamoto kubwa lakini tofauti na wenzetu ambao wao mapema waliwahi kubaini sisi tukachelewa.Kwahiyo changamoto zilipoanza kuwa kubwa na mapokeo yameendelea kuwa hasi.

Amesisitiza umuhimu kuzungumza kuhusu afya ya akili kuanzia umri mdogo wakiwemo watoto na vijana ili wajue, kwani hiyo inasaidia kutengeneza sio tu mbinu za kujilinda lakini pia kujilinda wenyewe kwa wenyewe.

Wakati huo huo Mshauri wa wanafunzi katika Sekondari ya Mzizima Theresia Mwaijala ametoa pongezi kwa Jubilee Health Insurance kwa kuona umuhimu wa kutoa elimu ya afya ya akili kwa wanafunzi.

“Juhudi zinazofanywa na Jubilee Health Insurance ni nzuri, wamekuja shuleni kwetu kuzungumza na wanafunzi kuhusu afya ya akili kitu ambacho ni muhimu kwasababu tunafahamu changamoto ya afya ya akili zinaanza mapema kuanzia miaka 14.

Hivyo amesema vizuri watoto wakapewa uelewa ,wafundishwe ili waweze kujilinda lakini wakiona kama kuna dalili ambazo zinaweza kusababisha afya ya akili wachukue hatua

Amesisitiza mafunzo ya Jubilee Health Insurance kuhusu afya ya akili kwa ujumla yanafaida kubwa ikiwemo kupata uelewa, na ukiwa na uelewa utachukua hatua sahihi.”



Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma 

Waziri katika Ofisi ya Rais – Maendeleo ya Vijana, Joel Nanauka, amesema kuwa katika mwaka wa fedha 2026/2027, serikali itatekeleza mpango wake kwa kuzingatia vipaumbele vinne vikuu vinavyolenga kuimarisha maendeleo ya vijana nchini.

Akizungumza leo bungeni mjini Dodoma wakati akiwasilisha mpango na makadirio ya matumizi ya Ofisi ya Rais – Maendeleo ya Vijana, Nanauka alisema lengo kubwa la vipaumbele hivyo ni kuwawezesha vijana kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi, kijamii na kisiasa, pamoja na kuboresha ustawi wao kwa ujumla.

Kwa mujibu wa Nanauka, vipaumbele hivyo vitajikita katika maeneo yafuatayo:

Kwanza, kuimarisha ukuzaji wa biashara na uwezeshaji wa vijana kiuchumi, kwa lengo la kuwasaidia vijana wengi zaidi kujiajiri na kuajiriwa katika sekta za biashara na uzalishaji.

Pili, kuimarisha uratibu na ushirikishwaji wa vijana katika masuala ya kijamii, kiuchumi na kisiasa ili kuongeza ushiriki wao katika maendeleo ya taifa.

Tatu, kuimarisha uratibu wa elimu ya uraia, uzalendo pamoja na usimamizi wa shughuli za Mwenge wa Uhuru nchini.

Nne, kuimarisha ustawi na makuzi bora ya vijana ili kuhakikisha wanakua katika mazingira yanayowawezesha kufikia ndoto zao na kuchangia maendeleo ya taifa.

Nanauka alisisitiza kuwa mpango huo ni sehemu ya juhudi za serikali kuhakikisha vijana wanakuwa nguzo muhimu ya maendeleo ya taifa kupitia fursa za kiuchumi na ushiriki mpana katika ujenzi wa nchi.



Na Janeth Raphael

Serikali kupitia Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo imesema kuwa mpango wa mkopo wa shilingi bilioni 20 uliotengwa kwa ajili ya kuwawezesha watengenezaji wa maudhui mitandaoni (content creators) umeonyesha mwitikio mkubwa kuliko ilivyotarajiwa, hali inayoashiria ongezeko kubwa la vijana wanaojihusisha na sekta ya ubunifu wa kidigitali nchini.

Akizungumza leo jijini Dar es Salaam wakati wa hafla ya utiaji saini wa makubaliano ya Tanzania kuwa mwenyeji wa Mashindano ya 74 ya Miss World 2027, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda, amesema lengo la mkopo huo ni kuwawezesha vijana wenye vipaji lakini wenye changamoto za kifedha ili waweze kukuza ubunifu wao na kujiajiri kupitia maudhui ya kidigitali.

Makonda amesema mpango huo ulipangwa kwa nia ya kuwasaidia vijana wanaoanza safari yao ya ubunifu, hasa wale wanaokosa vifaa muhimu kama kamera bora, vifaa vya uhariri, na rasilimali nyingine za msingi zinazohitajika katika uzalishaji wa maudhui ya kisasa.

Hata hivyo, amesema tathmini ya awali imeonesha kuwa maombi yamezidi kiwango kilichotarajiwa, jambo linaloonesha wazi kuwa sekta ya content creation imekuwa na mvuto mkubwa na inakua kwa kasi nchini Tanzania.

“Hatuwezi kuchukua mkopo huu tukawapa watu ambao tayari wana uwezo mkubwa, kama kumiliki magari ya gharama kubwa au kuwa na vifaa vya kisasa. Dhamira yetu ni kumsaidia kijana wa kawaida aliye mtaani, mwenye ndoto lakini hana uwezo wa kuanza,” amesema Makonda.

Kutokana na hali hiyo, Waziri huyo amesema serikali imeamua kuahirisha kwa muda utekelezaji wa mpango huo ili kufanya maboresho muhimu, yakiwemo marekebisho ya vigezo na masharti ya mkopo huo ili kuhakikisha unawafikia walengwa sahihi.

Ameongeza kuwa maboresho hayo yatalenga pia kuweka riba nafuu na masharti rahisi zaidi ili kuhakikisha mkopo huo hauwi mzigo kwa vijana, bali unakuwa kichocheo cha ukuaji wa sekta ya ubunifu na ajira nchini.

Serikali imesisitiza kuwa dhamira yake ni kuhakikisha vijana wengi zaidi wananufaika na fursa zilizopo kwenye uchumi wa kidigitali, ambao kwa sasa unaendelea kukua kwa kasi na kutoa nafasi kubwa za ajira na ubunifu.


Na Janeth Raphael- MichuziTv -Dodoma .

Serikali imetangaza mpango wa kuanzisha utafiti maalum utakaoweka msingi wa uanzishwaji wa Benki ya Vijana, hatua inayolenga kuboresha upatikanaji wa huduma za kifedha kwa vijana na kuondoa changamoto zinazowakabili katika kupata mikopo na mitaji ya biashara.

Akizungumza Bungeni jijini Dodoma leo Jumatatu, wakati akiwasilisha makadirio ya bajeti ya Wizara ya Maendeleo ya Vijana kwa mwaka wa fedha 2026/27, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais anayeshughulikia vijana, Mhe. Joel Nanauka, amesema utafiti huo utaanza rasmi katika mwaka huo wa fedha.

Amesema lengo kuu ni kubaini muundo sahihi wa taasisi hiyo ya kifedha ambayo itakuwa maalum kwa vijana, ili kuhakikisha inazingatia mazingira yao, uwezo wao wa kiuchumi na mahitaji halisi ya soko la ajira na uwekezaji.

Kwa mujibu wa Waziri Nanauka, Benki ya Vijana itakuwa chombo cha kimkakati kitakachosaidia kukuza ubunifu katika huduma za kifedha, kuongeza fursa za uwekezaji kwa vijana na kuchochea ajira mpya nchini. Pia, itasaidia kujenga mfumo imara wa kifedha unaojumuisha makundi yote ya vijana bila vikwazo vya kimtaji.

Aidha, serikali imeeleza kuwa itaendelea kuimarisha programu za mafunzo ya ujasiriamali na usimamizi wa biashara kwa vijana, sambamba na kuongeza upatikanaji wa mikopo nafuu kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Vijana ili kuwawezesha kujiajiri na kuajiri wengine.

Katika hatua nyingine, Waziri huyo amesema serikali pia inapanga kufanya utafiti wa kuanzisha Vituo vya Ubunifu kwa Vijana (Youth Innovation Hubs) vitakavyolenga kukuza vipaji, ubunifu na mawazo ya kibiashara. Vituo hivyo vitakuwa kiunganishi kati ya vijana na masoko, teknolojia pamoja na mitaji.

Pia, serikali itakuja na mfumo wa kitaifa wa kuratibu masuala ya maendeleo ya vijana pamoja na kuanzisha kanzidata ya taifa itakayokusanya taarifa muhimu za vijana ili kusaidia kupanga na kutekeleza sera kwa ufanisi zaidi.

Vilevile, mapitio ya sheria ya Baraza la Vijana yanatarajiwa kufanyika ili kuliboresha zaidi katika kusimamia na kuwakilisha maslahi ya vijana nchini.

Serikali imeeleza kuwa hatua hizi zote zinalenga kuongeza ushiriki wa vijana katika uchumi na kuhakikisha wanakuwa sehemu muhimu ya maendeleo ya taifa kupitia mfumo jumuishi wa kiuchumi na kijamii.


Serengeti. Serengeti Premium Apple imeandika historia kwa kuwasilisha uzinduzi wa kipekee ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, ikiweka alama kama kinywaji premium (RTD) cha kwanza kutengenezwa Tanzania na kampuni ya Serengeti Breweries Limited (SBL).

Kupitia matukio ya uzinduzi kwa siku tatu mfululizo, zaidi ya mastaa na watengeneza maudhui 30 kutoka sekta mbalimbali za ubunifu walisafirishwa kwa ndege binafsi kutoka Dar es Salaam mpaka Serengeti, wakipata fursa ya kushiriki na kufurahia matukio ya kipekee yaliyounganisha na ladha laini na ya kuburudisha ya kinywaji hicho, utamaduni na mandhari ya asili ya Tanzania.

Safari hiyo ilijumuisha matukio mbalimbali yaliyopangiliwa kwa ustadi na ubunifu, kuanzia mkutano na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, safari ya ndege binafsi angani, mpaka mapokezi ya kipekee ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Serengeti. Mastaa hao walipata nafasi ya kushiriki shughuli kama vile kutembelea na kujionea mbuga, chakula cha mchana (brunch) na cha jioni (dinner) katika mazingira ya kuvutia kilichoambatana na tafrija fupi. 

Siku iliyofuatia walishiriki kwa pamoja tukio la kipekee la “Toast in the Sky” lililofanyika kupitia ‘hot air balloon’ juu ya anga la Serengeti. Wageni waalikwa waliandaliwa shughuli tofauti zinazoonyesha namna kinywaji hiki kipya kinavyoweza kuakisi ubora na maisha ya kisasa yenye hadhi ya kimataifa.

Uzinduzi huu uliakisi kwa vitendo misingi mikuu ya chapa mpya ya Serengeti Premium Apple, ikiwemo ladha laini na ya kuburudisha ya apple; fahari ya bidhaa ya Kitanzania inayowakilisha ubunifu, usasa na mafanikio ya Mtanzania wa kisasa; pamoja na kuhamasisha Watanzanie kuendele kuvumbua na kufurahia uzuri na maeneo mapya nchini, ladha mpya na mtazamo mpya wa maisha.

Kupitia uzinduzi huu, kampuni ya Serengeti Breweries Limited imeonyesha uwezo wa Tanzania kutengeneza bidhaa zinazokidhi viwango vya kimataifa huku ikitumia utajiri wa rasilimali zilizopo kama jukwaa la kuonesha ubunifu na hadhi ya juu.






































Waziri wa Fedha Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akichangia mada katika mkutano ulioangazia umuhimu wa sekta ya maji katika maendeleo ya watu na uchumi wa dunia, chini ya kauli mbiu “usalama wa maji kwa mustakabali wa bara la Afrika: mtazamo wa mbele” ulioandaliwa na Benki ya Dunia, pembezoni mwa mikutano ya majira ya Kipupwe ya Benki hiyo na Shirika la Fedha la Kimataifa-IMF, uliofanyika jijini Washington D.C, nchini Marekani.
(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, WF, Washington D.C, Marekani)

Na Benny Mwaipaja, Washington D.C
WAZIRI wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), amesisitiza umuhimu wa nchi za Afrika kuweka mipango ya kuhakikisha kuwa maji salama yanapatikana kwa ajili ya matumizi ya binadamu na shughuli za kiuchumi lakini pia kulinda vyanzo vya maji.

Mhe. Balozi Omar alisema hayo wakati akichangia mada katika mkutano ulioangazia umuhimu wa sekta ya maji katika maendeleo ya watu na uchumi wa dunia, chini ya kauli mbiu “usalama wa maji kwa mustakabali wa bara la Afrika: mtazamo wa mbele” ulioandaliwa na Benki ya Dunia, pembezoni mwa mikutano ya majira ya Kipupwe ya Benki hiyo na Shirika la Fedha la Kimataifa-IMF, uliofanyika jijini Washington D.C, nchini Marekani.

Akijibu swali la namna rasilimali za maji zinavyoweza kulindwa na kutumika kama rasilimali za kiuchumi, Mhe. Balozi Omar alisema ni muhimu ieleweke kwamba maji ni rasilimali muhimu hivyo ni lazima kufanya utafiti wa kutambua vyanzo vya maji vilivyopo ikiwemo mito na maziwa na kuweka utekelezaji wake kwenye mipango ya kitaifa ya maendeleo ya muda mfupi, wa kati na muda mrefu.

“Pia ni muhimu kuvifuatilia na kuvilinda vyanzo hivyo na kuzitumia rasilimali hizo kwa uangalifu mkubwa ili tuendelee kuwa na maji safi, kuvilinda vyanzo hivyo dhidi ya uvamizi na uchafuzi wa maji, pamoja na kuondoa upotevu wa maji.” Alisema Mhe. Balozi Omar

Alitahadharisha kuwa idadi ya watu inaendelea kuongeza kwa kasi barani Afrika hatua iliyosababisha kuwa na uhitaji mkubwa wa maji na kushauri kuwepo kwa ushirikiano madhubuti kati ya sekta binafsi na wadau wengine wa maendeleo kama Benki ya Dunia ili kuwezesha upatikanaji wa rasilimali fedha kwa ajili kutekeleza mira ya maji.

Mkutano huo wa maji uliwashirikisha Mawaziri wa Fedha na wadau wengine kutoka nchi wanachama wa Benki ya Dunia kutoka baadhi ya nchi za Bara la Afrika ambapo walijadili namna sera, uwekezaji, mabadiliko ya kimfumo wa kitaasisi unavyoweza kuboresha na kuongeza upatikanaji wa maji safi na salama barani Afrika.



Na Mwamvua Mwinyi, Chalinze, Aprili 19, 2026
MWENGE wa Uhuru umetambua mchango wa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora,ambae pia ni Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete, kufuatia kuandika kitabu(andiko) kinachoelezea falsafa ya Mwenge wa Uhuru tangu kuanzishwa kwake mwaka 1961.

Imeelezwa Juhudi hizo za Ridhiwani, amezifanya wakati alipokuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, kuandika andiko hilo rasmi Kiserikali.

Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2026, Wazo Mwang’onda, alitambua mchango huo kuwa sehemu ya historia ya Taifa wakati wa mapokezi ya Mwenge wa Uhuru yaliyofanyika Aprili 19, 2026 katika Shule ya Msingi Kiwangwa, Halmashauri ya Chalinze, ukitokea Halmashauri ya Bagamoyo.

Mbali ya hilo, Ridhiwani ametajwa kuwa miongoni mwa wananchi wawili wa wilayani Bagamoyo waliotoa mchango wa kipekee kwa jamii, ambapo mmoja alijitolea kuvusha watoto darajani kwenda shule, huku mwingine akitoa eneo kwa ajili ya ujenzi wa shule.

Mwang'onda alieleza, Mwenge wa Uhuru ni moja ya tunu kubwa za Taifa, ukiwa kichocheo muhimu cha maendeleo, hususan katika kupambana na ujinga, maradhi na umaskini.

Awali, akipokea Mwenge huo, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Chalinze, Ramadhan Possi, alieleza jumla ya miradi saba yenye thamani ya sh. bilioni 34.179 inapitiwa, ambapo miradi mitatu imezinduliwa, mitatu imekaguliwa na mmoja umetembelewa.

Wakati huohuo, Mwang’onda ameridhishwa na utekelezaji wa mradi wa jengo la wagonjwa wa nje (OPD) katika Kituo cha Afya Kiwangwa uliogharimu shilingi milioni 20.583.

Pia Mwenge wa Uhuru umetembelea ujenzi wa boksi kalvati katika barabara ya Mwinyi–Kudiembe, Kata ya Bwilingu, uliotekelezwa kwa gharama ya shilingi milioni 67.3 kupitia TARURA; na kutembelea kiwanda cha Starlinkgulf Trading Co. Ltd (Wallput) kilichojengwa kwa gharama ya zaidi ya sh bilioni 34.

*Awataka wahakikishe miradi inasimamiwa na kuleta tija iliyokusudiwa

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema watendaji wa Serikali wanajukumu la kuhakikisha miradi ya maendeleo inayotokelezwa katika maeneo mbalimbali nchini ikiwemo ya maji, umeme, afya, miundombinu na elimu inasimamiwa ipasavyo ili Watanzania waweze kupata tija iliyokusudiwa.

Waziri Mkuu amesema Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameweka jitihada kubwa katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo, hivyo ni lazima itekelezwe kama ilivyokusudiwa.

Ametoa kauli hiyo leo (Jumapili, Aprili 19, 2026) wakati akizungumza na wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye uwanja wa Shule ya Msingi Msanga, Chamwino mkoani Dodoma baada ya kuweka jiwe la msingi mradi wa maji akiwa katika ziara ya kikazi ya kukagua miradi ya maendeleo.

Mheshimiwa Dkt. Mwigulu amesema jukumu kubwa walilonalo watendaji ni kusimamia ipasavyo miradi mbalimbali ya maendeleo inayotekelezwa katika maeneo yao na kuhakikisha wananchi wananufaika kama ilivyokusudiwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Waziri Mkuu amesema lengo la Serikali ni kuhakikisha Watanzania wote wananufaika na rasilimali za Taifa kupitia miradi mbalimbali ya maendeleo inayotekelezwa katika maeneo yao. “…Watanzania waweze kunufaika na matunda ya Taifa lao.”

Pia, Waziri Mkuu amewaasa Watanzania kujiepusha na watu wanaotumia kivuli cha imani za dini kufanya siasa za majukwaani, huku wakiwa na lengo ovu la kuwagawa watanzania kwa chuki za kiiimani na itikadi za kisiasa. “Ndugu zangu Watanzani tuendelee kulinda umoja na amani yetu. Kuna watu sasa wanatafuta namna ya kutumia siasa na dini ili kutugawa, tujihadhari na watu wa namna hiyo” amesisitiza.

Awali,Waziri Mkuu aliweka jiwe la msingi la mradi wa Maji wa Miji 28 wilayani Chamwino, ambapo alitumia fursa hiyo kumshukuru Mheshimwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa utekelezaji wa mradi huo akisema ni wa kimkakati unaokwenda kumaliza tatizo la maji katika maeneo hayo.

Kwa upande wake, Waziri wa Maji, Jumaa Aweso alisema Wizara ya Maji itahakikisha mradi huo mkubwa unakamilika kwa wakati ili wananchi waweze kunufaika. “Kupitia Wakala wa Maji Vijijini (RUWASA), Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameweka fedha nyingi na tayari vijiji 10,758 vimeshafikiwa na huduma ya maji safi na salama na vimebakia vijiji 1,575.”

Akitoa taarifa ya mradi huo Mkurugenzi wa Usambazaji wa Maji Mijini kutoka Wizara ya Maji, Mhandisi Charles Mafie alisema kwamba mkataba wa mradi huo unatarajiwa kukamilika Agosti 10, 2026 ukiwa na thamani ya shilingi Bilioni 17.2 na umefikia asilimia 70.2 ya utekelezaji.

Mradi huo unatarajiwa kuhudumia zaidi ya wananchi 60,000 katika kata za Msanga, Buigiri, Chamwino na Mtumba na kuongeza upatikanaji wa maji safi kutoka asilimia 91 hadi 100 pamoja na kuimarisha uzalishaji wa maji kukidhi mahitaji ya sasa na ya baadae.

Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma 

WAZIRI Mkuu wa Tanzania, Dkt Mwigulu Nchemba, ametoa onyo kali kwa watu wanaodaiwa kuwa na njama za kuvuruga amani ya nchi, akiwataka Watanzania wote kuendelea kuwa walinzi wa kwanza wa utulivu na mshikamano wa taifa. Amesema kuwa amani ya Tanzania si jambo la kubahatisha, bali ni tunu inayopaswa kulindwa kwa nguvu zote na kila mwananchi.

Akizungumza jijini Dodoma, katika wilaya ya Chamwino, Dkt Mwigulu alionyesha msimamo thabiti wa serikali katika kuhakikisha hakuna mtu au kundi litakaloruhusiwa kuchezea amani ya nchi. Amesisitiza kuwa vyombo vya dola viko macho na vitachukua hatua kali dhidi ya yeyote atakayebainika kuhatarisha usalama na utulivu wa taifa.

Mbali na hilo, Waziri Mkuu ameelekeza ujumbe kwa viongozi wa umma, akiwataka kufanya kazi kwa weledi, uaminifu na uwajibikaji wa hali ya juu. Amekemea vikali vitendo vya rushwa na matumizi mabaya ya madaraka, akisisitiza kuwa serikali haitamvumilia kiongozi yeyote atakayekiuka maadili ya utumishi wa umma.

Amefafanua kuwa anafuatilia kwa karibu utekelezaji wa miradi yote ya maendeleo nchini ili kuhakikisha thamani ya fedha inaonekana kwa wananchi. “Kila mradi ninaangalia, kila hatua inafuatiliwa. Atakayekwenda kinyume, hatabaki salama kwenye nafasi yake,” alisisitiza, akionyesha dhamira ya serikali kusimamia rasilimali za umma kwa umakini mkubwa.

Dkt Mwigulu amegusia pia suala la haki kwa wananchi, akionya kuwa hatasita kuwachukulia hatua wale wote wanaowaonea wengine au kukandamiza haki za wananchi. Kauli yake ya, “Wale wanaowaonea wengine nitashughulika nao, msiwe na mashaka — upele umepata mkunaji,” ilizua hisia za matumaini kwa wananchi kuhusu hatua madhubuti zitakazochukuliwa dhidi ya vitendo vya dhuluma.

Aidha, amewahimiza wananchi kuendelea kushirikiana na serikali katika kulinda rasilimali za taifa na kuhakikisha maendeleo yanawafikia wote kwa usawa. Amesisitiza kuwa maendeleo ya kweli hayawezi kupatikana bila kuwepo kwa amani, nidhamu na uwajibikaji wa pamoja.

Kauli hizo zinakuja wakati serikali ikiendelea kuimarisha misingi ya utawala bora, kupambana na rushwa, na kusukuma mbele ajenda ya maendeleo kwa lengo la kujenga taifa lenye uchumi imara na ustawi wa wananchi wake.













Na Pamela Mollel,Arusha

Mashindano ya Tanfom Marathon yamefanyika kwa mafanikio makubwa jijini Arusha, yakiambatana na maadhimisho ya miaka 60 tangu kuanzishwa kwake, tukio ambalo limeendelea kuipa heshima Tanzania katika sekta ya michezo na kuvutia wanariadha kutoka ndani na nje ya nchi.

Akizungumza katika mashindano hayo, Rais wa Shirikisho la Riadha Tanzania, Rogath John, amesema mashindano hayo yameonesha kiwango kikubwa cha ushindani na maandalizi bora kutoka kwa wanariadha, jambo linaloonesha maendeleo ya riadha nchini.

Amesema Tanfom Marathon ni sehemu muhimu ya maandalizi ya wanariadha kuelekea mashindano ya kimataifa, akibainisha kuwa lengo la shirikisho ni kuona Tanzania inazidi kuongeza ushindani na kupata medali zaidi katika mashindano makubwa duniani.

Kwa upande wa wadhamini, Meneja wa Kanda ya Kaskazini wa CRDB Bank, Cosmas Sadat, amesema benki hiyo itaendelea kuunga mkono matukio ya michezo na kijamii kama sehemu ya kurudisha kwa jamii.

Amesema uwekezaji katika michezo unachochea afya bora, mshikamano wa jamii na pia kukuza fursa za kiuchumi kupitia michezo na utalii wa michezo.

Mashindano hayo ya kilomita 42 yamehusisha wanariadha kutoka mataifa mbalimbali ikiwemo Kenya, Uganda na Uholanzi, hali iliyoongeza ushindani na hadhi ya kimataifa ya tukio hilo lililofanyika Arusha.

Wanariadha wa ndani na nje walionesha kiwango kikubwa cha ushindani, hali iliyoifanya Tanfom Marathon kuendelea kuwa moja ya mashindano yenye hadhi kubwa nchini.

Kwa upande wa wanaume, Modest Petro Kalist ameibuka mshindi wa kwanza baada ya kuonesha kiwango cha juu cha mbio na uthabiti mkubwa. Kalist amesema ushindi huo umetokana na mazoezi ya muda mrefu na uzoefu wa mashindano ya awali, yaliyomsaidia kukabiliana na ushindani mkali kutoka kwa wanariadha wa kimataifa.

Kwa upande wa wanawake, Vaileth Adam ameibuka mshindi wa kwanza wa kilomita 42, akionesha nidhamu, uvumilivu na maandalizi mazuri yaliyomuwezesha kufanikiwa. Amesema ushindani wa kimataifa ulimpa motisha zaidi ya kuongeza juhudi na kuwahimiza vijana kuendelea kujituma katika michezo.

Katika mashindano hayo, washindi wamepatiwa zawadi mbalimbali ikiwemo fedha taslimu, ambapo mshindi wa kwanza amepata shilingi milioni 6, huku washiriki wengine wakipatiwa zawadi tofauti ikiwemo magodoro kama sehemu ya kutambua juhudi zao.

Wadau wa michezo wamesema Tanfom Marathon imeendelea kuwa moja ya mashindano makubwa yenye mchango mkubwa katika kukuza riadha, kuimarisha afya za wananchi na kuitangaza Tanzania kimataifa kupitia michezo.

Kwa ujumla, maadhimisho ya miaka 60 ya Tanfom Marathon yameacha historia kubwa jijini Arusha, yakionesha ukuaji wa riadha nchini na kuimarika kwa ushiriki wa kimataifa.








Na Asia Singano na Josephine Majura, WF, Mwanza.
SERIKALI imeeleza dhamira yake ya kuendelea kuwawezesha vijana kiuchumi kupitia sera na mipango mbalimbali ya kiuchumi na kijamii.

Hayo yameelezwa na Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb), katika Mahafali ya 20 ya Shule ya Sekondari ya Thaqaafa, wilayani Nyamagana mkoani Mwanza.

Alieleza kuwa, Serikari inaendelea kuweka mazingira wezeshi kwa vijana kupitia Sera na mipango mbalimbali ya kiuchumi na kijamii ili kuhakikisha kuwa vijana wanapata fursa za kuendeleza vipaji vyao na kuchangia kikamilifu maendeleo ya taifa.

‘’Dunia ya sasa inahitaji vijana wanaoweza kutatua changamoto kwa ubunifu, hasa katika nyanja za uchumi, teknolojia na ujasiriamali ‘’ Alisema Mhe. Munde (Mb).

Amewaasa vijana kuendelea kuwa na nidhamu na uadilifu kwakuwa Taifa linahitaji vijana wenye misingi imara ya maadili, wanaoweza kusimamia rasilimali za nchi kwa uwajibikaji na weledi.

Kwa upande wake Meneja wa Shule ya Thaqaafa, Bw. Idrisa Hayeshi, amewasisitiza wazazi kuendelea kushirikiana na walimu na Uongozi wa shule kufuatilia maendeleo ya wanafunzi ili kujua mwenendo wa tabia ambazo zina athari katika masomo yao.

“Shule imejipanga kutoa elimu bora ikiwa na matokeo mazuri kwa kila mwaka, tunavyofanya mawasiliano na mzazi ni kwamba atoe ushirikiano ili mtoto apate kitu kinachostahili’’ alisema Bw. Hayeshi.

Shule ya Sekondari Thaqaafa imeadhimisha Mahafali ya 20 ya Kidato cha Sita ambayo yalihudhuriwa na wahitimu (50).
Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima akipokea picha yake iliyochorwa wakati wa uzinduzi wa Binti Jasiri UDSM inayoongozwa na kaulimbiu isemayo Weka Malengo, Piga Hatua Timiza Malengo uliofanyikakatika katika ukumbi wa Nkurumah.
Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima akipokea tuzo kutoka kwa Makamu wa Rais wa Serikali ya Wanafunzi wa Joyce Juliasi Semkuyu, katika ukumbi wa Nkrumah. Tuzo hii ni ishara ya kutambua mchango wake katika jamii na juhudi zake za kuhamasisha maendeleo, hususan kwa wanawake.

Na Mwandishi Wetu WMJWM- Dar Es Salaam
WAZIRI wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima amewataka watoto wa kike kujipambanua katika kuhakikisha wanatumia muda wao kufanya mambo yatakayowasaidia katika ustawi wa maisha yao.

Waziri Dkt. Gwajima ameyasema hayo tarehe 18 Aprili, 2026 wakati akizindua Binti Jasiri UDSM inayoongozwa na kaulimbiu isemayo Weka Malengo, Piga Hatua Timiza Malengo.

Waziri Gwajima amesema jina la Binti Jasiri lina maana kubwa sana likiwakilisha ujasiri wa kusimama, kuota ndoto kubwa na kushinda changamoto hivyo katika ulimwengu wa leo, kunahitajika kuwa na mabinti ambao hawataogopa kushika nafasi za uongozi, kuanzisha biashara, wala kuchangia katika maamuzi makubwa ya kijamii na kiuchumi.

Ameeleza kuwa mpango huo umejengwa katika msingi imara unaoendana na dira ya maendeleo ya taifa yaani Dira ya Maendeleo ya Tanzania 2025, pamoja na malengo ya kimataifa ya maendeleo endelevu, hasa Elimu Bora (SDG 4) na Usawa wa Kijinsia (SDG 5).

“Binti Jasiri si tukio la siku moja bali ni mwanzo wa harakati endelevu na ni mwanzo wa kizazi kipya cha wanawake; Wenye maono, ujasiri na uwezo wa kubadilisha dunia.” Ameafafnua Waziri Dkt Gwajima.

Aidha amesema licha ya mafanikio yaliyopatikana, bado mabinti wengi wanakutana na changamoto mbalimbali ikiwa ni pamoja na ukosefu wa mentorship, fursa za uongozi na rasilimali za kujiendeleza hivyo kupitia Binti Jasiri, inaunda mazingira yatakayowawezesha mabinti kujifunza uongozi, kuunganishwa na wale waliowatangulia na kujenga ujasiri wa kujitegemea na hatimaye kuwa suluhisho la changamoto za jamii.

“Nitoe wito kwa Mabinti wangu wapendwa, nataka muondoke hapa leo mkiwa na jambo moja moyoni ambalo ni uwezo, thamani kwani unaweza kufika mbali zaidi ya unavyodhani pia usiruhusu hofu, maneno ya watu au mazingira yakuzuie kwani Dunia inahitaji sauti yako, mchango wako na uongozi wako basi chukua nafasi Jitokeze na Jiamini.” Amesisitiza Waziri Gwajima

Pia amewataka wadau wote wanaotokea serikalini, sekta binafsi, taasisi na washirika kusisitiza kuwa kuwekeza kwa mwanamke kwani ni uwekezaji kwa taifa na kumuinua msichana mmoja ni kuinua familia, jamii na uchumi mzima hivyo amewahimiza kuendelea kuunga mkono mipango kama hiyo kutoa mentorship na kufungua milango ya fursa kwa vijana wa kike.

Kwa upande wake Makamu wa rais wa Serikali ya Wanafunzi Chuo Kikuu cha Dar Es Salaam Joyce Juliasi Senkuli amesema Jukwaa hilo limeanzishwa kwa lengo la kumkomboa binti kifikra, kihisia, kielimu na kiuchumi, kwa kutambua kuwa bado wapo mabinti wengi wanaopitia changamoto mbalimbali katika safari ya maisha na elimu.

Naye Mwakilishi wa Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar Es Salaam Paulina Mabuga ameahidi kuwaunga mkono Mabinti hao ili waweze kufikia malengo yao katika kampeni walioianzisha ya kuwafanya Watoto wa kike kuinuka katika masuala mbalimbali katika jamii.

Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima akizungumza katika uzinduzi wa Binti Jasiri UDSM inayoongozwa na kaulimbiu isemayo Weka Malengo, Piga Hatua Timiza Malengo uliofanyika katika ukumbi wa Nkurumah. .
Baadhi ya Washiriki katika uzinduzi wa Binti Jasiri UDSM ulkofanywa na Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima katika ukumbi wa Nkurumah.

Top News