-Serikali  Yaendelea Kutenga Maeneo Mapya kwa Wachimbaji Wadogo, Leseni 108 Zatolewa

📍Dodoma,– 

Serikali imeendelea kuimarisha mazingira ya uwekezaji na ushiriki wa wananchi katika Madini kwa kuendelea kutenga maeneo maalum kwa ajili ya wachimbaji wadogo nchini, hatua inayolenga kuongeza fursa za ajira, kuinua uchumi wa wananchi na kurasimisha shughuli za uchimbaji mdogo. 

Katika utekelezaji wa hatua hiyo, Serikali tayari imetenga eneo la Nyakafulu, Wilaya ya Mbogwe Mkoani Geita kwa wachimbaji wadogo na kutoa leseni 108 baada ya kufutwa kwa leseni zilizokuwa haziendelezwi ipasavyo.

Hatua hiyo imebainishwa bungeni leo Mei 26, 2026 na Naibu Waziri wa Madini, Mhe. Dkt. Steven Kiruswa kwa niaba ya Waziri wa Madini wakati akijibu maswali ya wabunge kuhusu maendeleo ya Sekta ya Madini.

Akijibu swali la Mbunge wa Mbogwe, Mhe. Fagason Nkingwa aliuliza kuwa ni lini Serikali itatenga maeneo kwa wachimbaji wadogo na kuwapatia leseni za uchimbaji, Dkt. Kiruswa amesema Serikali tayari imetenga eneo la Nyakafulu kwa ajili ya wachimbaji wadogo na kutoa jumla ya leseni 108 baada ya kufutwa kwa leseni ambazo hazikuwa zimeendelezwa.

Amesema kuwa, hatua hiyo inaakisi dhamira ya Serikali ya kuendelea kurasimisha na kukuza shughuli za uchimbaji mdogo nchini ili wananchi wengi zaidi waweze kushiriki katika uchumi wa madini kwa tija na manufaa mapana.

“Serikali kupitia Tume ya Madini inaendelea kufanya tathmini ya kisheria ya leseni 63 za utafiti ambazo hazijaendelezwa ipasavyo kwa lengo la kuzifuta pale inapobidi na kuyatenga baadhi ya maeneo hayo kwa wachimbaji wadogo,” amesema Dkt. Kiruswa.

Aidha, Dkt. Kiruswa ameeleza kuwa Serikali itaendelea kuchambua taarifa za jiosayansi ili kubaini maeneo yenye tija kwa wachimbaji wadogo, huku Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) ikipewa jukumu la kufanya tafiti za kina kwenye maeneo yenye taarifa hafifu kabla ya kutengwa rasmi kwa shughuli za uchimbaji mdogo.

Katika hatua nyingine, Serikali imeeleza kuwa ipo katika hatua za mwisho za kukamilisha uhakiki wa madai ya waliokuwa watumishi wa Mgodi wa Kiwira kabla ya kuanza kulipa madeni hayo.

Akijibu swali la Mbunge wa Kyela, Mhe. Baraka Mwamengo kuhusu lini Serikali itawalipa waliokuwa watumishi wa Mgodi wa Kiwira, Dkt. Kiruswa ameeleza madai hayo yalitokana na malalamiko ya mapunjo ya mafao kwa wafanyakazi waliokuwa wakihudumu mgodini hapo kabla ya ubinafsishaji.

Amefafanua  kuwa baada ya malalamiko kuwasilishwa na Chama cha Wafanyakazi Migodini na Ujenzi (TAMICO), Serikali ilifanya ukaguzi maalum kupitia Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali mwaka 2008 na baadaye kufanya uhakiki mwingine mwaka 2015.

Kwa mujibu wa uhakiki huo, madai halali ya wafanyakazi 893 yalibainika kuwa shilingi bilioni 1.024 tofauti na madai ya awali ya zaidi ya shilingi bilioni 47 yaliyokuwa yakidaiwa na wafanyakazi 1,687. Aidha, kulikuwepo na madeni ya wazabuni mbalimbali yaliyofanya jumla ya deni kufikia shilingi bilioni 1.52.

Dkt. Kiruswa amesema Serikali tayari imejumuisha madeni hayo kwenye orodha ya madeni ya Serikali na kwamba Wizara ya Madini inaendelea kushirikiana na Wizara ya Fedha kuhakikisha malipo yanafanyika baada ya kukamilika kwa uhakiki wa mwisho unaoendelea kwa sasa.

“Kwa sasa timu ya wataalamu inakamilisha taarifa ya mwisho ya uhakiki ili madeni hayo yaweze kulipwa na Serikali,” amesisitiza Dkt. Kiruswa.



 Na Mwandishi Wetu

DAR ES SALAAM — Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Dkt. Dotto Kuhenga, amewapongeza Dkt. Frank Sanga na Dkt. Alex Benson baada ya kutunukiwa Shahada za Uzamivu (PhD) katika fani ya Uandishi wa Habari na Mawasiliano ya Umma, akieleza kuwa safari yao ni mfano wa uvumilivu, ustahimilivu na kujituma.

Dkt. Kuhenga alieleza hayo kupitia kurasa zake za kijamii akirejea tukio la Mei 25, 2026, ambapo wasomi hao walitunukiwa shahada hizo, akibainisha kuwa mafanikio yao ni ushuhuda kwamba juhudi na azma ya kufikia malengo huzaa matunda.

Akizungumzia uhusiano wake na Dkt. Frank Sanga, Dkt. Kuhenga alisema walifahamiana zaidi ya miaka 17 iliyopita katika Kampuni ya Mwananchi Communications Ltd, alipokuwa amejiunga kama mwandishi wa habari wa gazeti la The Citizen huku Dkt. Sanga akiwa Mhariri wa Mwanaspoti.

Alimuelezea Dkt. Sanga kuwa ni mtu mwenye upeo mkubwa wa kitaaluma, mwenye uzoefu mpana na mtazamo wa kimataifa katika tasnia ya habari.

Kuhusu Dkt. Alex Benson, alisema wamekuwa pamoja tangu walipokuwa wanafunzi wa shahada ya kwanza katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, na baadaye wakawa wahadhiri wenza chuoni hapo pamoja na kushirikiana katika miradi mbalimbali ya kitaaluma.

Aidha, Dkt. Kuhenga alisema safari za masomo ya uzamivu za wasomi hao zinatoa funzo kwa wengi kuwa kujituma na kuwa na msimamo katika kufikia malengo ni msingi muhimu wa mafanikio.

Pia alibainisha kuwa Dkt. Frank Sanga na Dkt. Alex Benson walifanyiwa usimamizi wa tafiti na Profesa Michael Andindilile, ambaye pia aliwahi kuwa msimamizi wake katika safari yake ya shahada ya uzamivu miaka iliyopita.

“Maisha ni mzunguko wa aina yake. Hongereni sana Dkt. Frank Sanga na Dkt. Alex Benson. Simulizi zenu ni chachu kwa wengi,” ameandika Dkt. Kuhenga.

 

Mwenyekiti wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB), Bw. Tido Mhando, amewataka Waandishi wa Habari nchini kutafakari upya wajibu wao katika kuijenga jamii kupitia maudhui yenye tija, akieleza kuwa ipo haja ya kurejesha hadhi na nguvu ya taaluma hiyo katika kujenga fikra na maendeleo ya taifa.

Akizungumza jijini Dar es Salaam, Bw. Mhando amesema pamoja na JAB kusimamia utoaji wa ithibati kwa kuzingatia vigezo vya elimu na sheria, bado kuna umuhimu wa Waandishi wa Habari kuendelea kujengewa uwezo kupitia mafunzo ya kitaaluma.

“Tukitazama baadhi ya vyombo vyetu vya habari, iwe ni magazeti, redio au televisheni, mambo ya kufikirisha kwa kiasi kikubwa yamepungua. Waandishi wa Habari wanapaswa kutafakari kama hiyo ndiyo taswira wanayotaka kuiacha katika jamii ya Watanzania,” amesema.

Amesisitiza kuwa vyombo vya habari vina nafasi kubwa ya kuunda mtazamo wa jamii, hivyo kuna wajibu wa kuhakikisha maudhui yanayotolewa yanajenga uelewa, yanakuza maendeleo na yanalinda maslahi ya taifa.

“Tunachosimamia ni kuhakikisha Mwandishi wa Habari anayepata ithibati anakuwa na kiwango cha elimu kisichopungua Diploma, lakini tunataka pia Waandishi wa Habari waendelee kupata mafunzo ili waweze kuimarika zaidi kitaaluma,” amesema.

Amesema ipo haja ya sekta ya habari kutafakari aina ya maudhui yanayopewa kipaumbele, akisisitiza kuwa vyombo vya habari vina nafasi kubwa katika kujenga fikra na mwelekeo wa jamii.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimuapisha Mhe. Rabia Hussein Mohamed kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani kwenye hafla iliyofanyika Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 26 Mei, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimuapisha Mhe. Dkt. Yose Joseph Mlyambina kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani kwenye hafla iliyofanyika Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 26 Mei, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimuapisha Mhe. Immaculata Kajetan Banzi kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani kwenye hafla iliyofanyika Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 26 Mei, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimuapisha Mhe. Cyprian Phocas Mkeha kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani kwenye hafla iliyofanyika Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 26 Mei, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimuapisha Mhe. Yohane Bokobora Masara kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani kwenye hafla iliyofanyika Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 26 Mei, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimuapisha Mhe. Dkt. Juliana Laurent Masabo kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani kwenye hafla iliyofanyika Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 26 Mei, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimuapisha Mhe. Abdi Shaaban Kagomba kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani kwenye hafla iliyofanyika Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 26 Mei, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimuapisha Mhe. Ibrahim Mzee Ibrahim kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani kwenye hafla iliyofanyika Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 26 Mei, 2026.

Waheshimiwa Majaji wa Mahakama ya Rufani wakiapa Kiapo cha Maadili kwenye hafla iliyofanyika Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 26 Mei, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na viongozi mbalimbali mara baada ya kuwaapisha Majaji 9 wa Mahakama ya Rufani, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 26 Mei, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na viongozi mbalimbali kwenye picha na Majaji wa Mahakama ya Rufani, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 26 Mei, 2026.


Na Mwandishi Wetu, Pwani

MPANGO wa Rafiki wa Binti umezindua wimbo maalumu wa  kielimu wa Afya ya Hedhi ikiwa ni kuelekea Maadhimisho ya Siku ya Afya ya Hedhi Mei 28, 2026.

Taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa na Saumu Zidadu, ambaye ni Mratibu wa Mpango wa Rafiki wa Binti, amesema pia wamepanua kuongeza usambazaji wa chupi maalumu za hedhi zinazoweza kutumika tena Tanzania.

“Katika kuadhimisha Siku ya Afya ya Hedhi tarehe 28 Mei, Rafiki wa Binti imetoa wimbo mpya wa kielimu wa uhuishaji unaolenga kuwapa wanafunzi wa kike elimu kuhusu afya ya hedhi pamoja na kuhamasisha kujiamini, heshima na mahudhurio shuleni.

“Wimbo huo umeimbwa na kuandikwa na mwimbaji maarufu wa Tanzania Ashura Kitenge, na ni sehemu ya mpango mpana wa elimu ya afya ya hedhi wa Rafiki wa Binti, ambao huwafundisha wasichana namna sahihi ya kutumia, kufua na kutunza chupi maalumu za hedhi zinazoweza kutumika tena suluhisho bunifu na endelevu linalowasaidia wasichana kujisimamia hedhi zao kwa usalama na kujiamini,”imesema taarifa hiyo ya Zidadu.

Kwa upande wake Nancy Bondo, ambaye ni Mkurugenzi wa Rafiki wa Binti, amesema chupi maalumu za hedhi zinazoweza kutumika tena, ni suluhisho jipya na la kipekee katika jamii nyingi za Tanzania na zimekuwa sehemu muhimu ya kazi ya Rafiki wa Binti katika kusaidia wasichana kuendelea na masomo yao na kupunguza unyanyapaa unaohusiana na hedhi.

“Kupitia mpango wake wa Pakiti za Binti, Rafiki wa Binti tayari imetoa zaidi ya jozi 24,000 za chupi maalumu za hedhi zinazoweza kutumika tena kwa wanafunzi wa kike katika maeneo ya Mafinga, Kilwa Masoko, Mkoa wa Kagera na Zanzibar. Chupi hizo zinaweza kutumika tena kwa miaka miwili au zaidi,” amesema na kuongeza:

Kila Pakiti ya Binti ina jozi sita za chupi maalum za hedhi zinazoweza kutumika tena, elimu ya afya ya hedhi, mifuko ya kuhifadhia vifaa vilivyo vikavu na vyenye unyevunyevu

“Jozi nyingine 24,000 za chupi zinatarajiwa kusambazwa katika utekelezaji wa programu zijazo ndani ya miezi michache ijayo wakati taasisi hiyo ikiendelea kupanua huduma zake kote nchini Tanzania. Afya ya hedhi inahusu elimu na fursa,” amesema Nancy Bondo. 

Amesema mrejesho kutoka serikalini, kwa walimu na wanafunzi kuhusu Mradi wa Binti umekuwa mazuri sana na unawasaidia wasichana kuendelea kuhudhuria shule wakati wa hedhi zao kwa heshima na kujiamini.

"Rafiki wa Binti inajivunia kuwa mshirika rasmi wa Siku ya Afya ya Hedhi na mwanachama wa Muungano wa Afya ya Hedhi Tanzania, ikifanya kazi pamoja na Serikali na wadau mbalimbali nchini kuboresha uelewa na upatikanaji wa huduma za afya ya hedhi,” amesema.

Amesema Rafiki wa Binti ni mpango unaolenga Tanzania, unaosaidia wasichana kupitia elimu ya afya ya hedhi na utoaji wa chupi maalum za hedhi zinazoweza kutumika tena ili kuwasaidia wasichana kubaki shuleni, kuwa na nguvu na kujiamini.

Amesema Rafiki wa Binti ni programu ya Rafiki Australia Tanzania, taasisi inayoendeshwa kwa kujitolea kwa asilimia 100 na iliyosajiliwa Australia na Tanzania.





Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma 

Serikali kupitia Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora imewataka Wakuu wa Idara za Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu katika taasisi za umma kuhakikisha wanashiriki wenyewe katika kikao kazi cha kitaifa kitakachofanyika jijini Dodoma kuanzia Juni 1 hadi 3, 2026, bila kukosekana wala kutuma wawakilishi.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma, Katibu Mkuu wa Ofisi hiyo, Juma Mkomi amesema kikao hicho ni muhimu katika kuimarisha ufanisi wa utendaji wa rasilimaliwatu serikalini, hivyo kinahitaji ushiriki wa moja kwa moja wa viongozi wote husika.

Amesema kikao hicho kitawakutanisha Wakurugenzi na Wakuu wa Idara za Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu kutoka Wizara mbalimbali, Idara zinazojitegemea, Wakala za Serikali, Mashirika ya Umma, Sekretarieti za Mikoa pamoja na Mamlaka za Serikali za Mitaa, kwa lengo la kujadili mikakati ya kuongeza uwajibikaji, ufanisi na nidhamu ya utendaji katika Utumishi wa Umma.

Mkomi amesema kikao hicho kitafanyika katika Ukumbi wa Mabele Hall jijini Dodoma chini ya kaulimbiu isemayo:

“Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu katika Utumishi wa Umma Ulio Sikivu, Jumuishi, wenye Matokeo na Uwajibikaji Kuelekea Dira 2050.”

Amefafanua kuwa moja ya ajenda kuu zitakazojadiliwa ni matumizi ya mifumo ya kidijiti katika usimamizi wa rasilimaliwatu, ikiwemo mifumo ya e-Uhamisho, e-Watumishi, e-Utendaji, e-Mrejesho pamoja na HR Assessment, ambayo inalenga kuongeza uwazi, ufanisi na uwajibikaji katika taasisi za umma.

Kwa mujibu wa Katibu Mkuu huyo, mifumo hiyo ya kidijiti ni sehemu ya maboresho makubwa yanayoendelea serikalini ili kuendana na mabadiliko ya kiteknolojia pamoja na kutimiza vipaumbele vya Taifa kuelekea Dira ya Maendeleo 2050.

Aidha, amesisitiza kuwa viongozi wote watakaohudhuria watapatiwa maelekezo mahsusi kuhusu usimamizi bora wa rasilimaliwatu serikalini, huku akibainisha kuwa hakutakuwa na nafasi ya uwakilishi, kutokana na umuhimu na uzito wa maudhui yatakayojadiliwa katika kikao hicho.

“Ni muhimu kila kiongozi anayehusika kuhudhuria mwenyewe ili kupata uelewa wa moja kwa moja na maelekezo ya kimkakati kuhusu maboresho ya sekta ya rasilimaliwatu,” ameweka msisitizo Mkomi.

Vilevile, kikao hicho kinatarajiwa kufunguliwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Ridhiwani Jakaya Kikwete, ambaye anatarajiwa kutoa mwelekeo wa serikali kuhusu maboresho ya utumishi wa umma na usimamizi wa rasilimaliwatu nchini.

Serikali imesema kikao hicho ni sehemu ya juhudi za kuimarisha utawala bora, kuongeza uwajibikaji wa watumishi wa umma na kuhakikisha taasisi za serikali zinaendeshwa kwa ufanisi unaozingatia matokeo.





Na Mwandishi Wetu

BABATI — Mahakama ya Mwanzo Wilaya ya Babati mkoani Manyara imesitisha kusikiliza kesi ya jinai namba 291 ya mwaka 2026 iliyofunguliwa na aliyekuwa Mbunge wa Babati Mjini, Paulina Gekul, inayomkabili Brayton Lucas (17), baada ya kujiridhisha kuwa mshtakiwa huyo ni mtoto mwenye umri wa chini ya miaka 18 na hivyo shauri hilo linapaswa kusikilizwa katika Mahakama ya Watoto kwa mujibu wa sheria.

Uamuzi huo ulitolewa baada ya Wakili wa upande wa utetezi, Thadei Lister, kuiomba mahakama kujiridhisha kuhusu umri wa mshtakiwa kwa kuwasilisha nyaraka mbalimbali ikiwemo cheti cha kuzaliwa kilichoonesha kuwa Brayton alizaliwa Novemba 12, 2008 na kwa sasa ana umri wa miaka 17 na miezi sita, tofauti na taarifa zilizokuwa katika hati ya mashtaka zilizomtaja kuwa na miaka 19.

Katika shauri hilo, Paulina Gekul alidai kuwa Brayton Lucas, ambaye alikuwa akichunga mifugo yake, alihusika katika wizi wa mbuzi 15 wenye thamani ya shilingi milioni tatu, kosa linalodaiwa kufanyika chini ya kifungu cha 268 cha sheria ya wizi wa mifugo. Kesi hiyo ilikuwa na jumla ya watuhumiwa watatu.

Mahakama pia ilielezwa kuwa mtoto huyo alikuwa amechanganywa katika shauri moja na watuhumiwa watu wazima, jambo ambalo upande wa utetezi ulidai ni kinyume na sheria zinazolinda haki za mtoto.

Baada ya kupitia nyaraka zilizowasilishwa, Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo Babati, Ahmed Mgodo, alisema mahakama imejiridhisha kuwa Brayton Lucas ni mtoto na hivyo haina mamlaka ya kuendelea kusikiliza kesi hiyo. Kutokana na uamuzi huo, mahakama ilisimamisha shauri hilo dhidi ya mshtakiwa huyo na kuagiza polisi kuandaa hati mpya ya mashtaka kwa mujibu wa sheria zinazohusu watoto.

Brayton Lucas alipatiwa dhamana huku washtakiwa wawili wengine wakiendelea kushikiliwa. Wakili Thadei Lister amesema wako tayari kuendelea kumtetea mtoto huyo iwapo atafikishwa katika Mahakama ya Watoto.

Akizungumza nje ya mahakama, Wakili Thadei alisema Brayton ni mwanafunzi wa kidato cha nne ambaye alitoweka akiwa Wilaya ya Arumeru mkoani Arusha na wazazi wake walikuwa wakimtafuta kwa kipindi cha miezi mitatu kabla ya kupata taarifa kuwa amekamatwa Babati kwa tuhuma za wizi.

Mama mzazi wa Brayton alisema mtoto wake alitakiwa kuwa shuleni baada ya kumaliza kidato cha nne na tayari alikuwa amepangiwa shule, lakini aliondoka nyumbani bila kutoa taarifa na baada ya juhudi za muda mrefu za kumtafuta walipata taarifa kuwa alikuwa Babati akifanya kazi.

Wakati huo huo, Diwani wa Kata ya Maruvango Wilaya ya Arumeru Mashariki, Digna Nassari, amesema taarifa za kupotea kwa mtoto huyo zilikuwa zimetolewa polisi miezi mitatu kabla ya kufunguliwa kesi dhidi yake na Paulina Gekul.

Aidha, Digna amesema Brayton ni miongoni mwa watoto 16 kutoka kata hiyo waliotoroka shule, huku akisisitiza umuhimu wa jamii kushirikiana kuhakikisha watoto wanarudi katika mfumo wa elimu na kupata ulinzi unaostahili.

Na Mwandishi wetu - Msumbiji

Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Dkt. Jim Yonazi ameupongeza Ubalozi wa Tanzania nchini Msumbiji kwa namna unavyoendelea kutekeleza majukumu yake na kuimarisha mahusiano baina ya nchi hizo mbili.

Ametoa pongezi hizo alipotembelea ofisi hizo pamoja na ujumbe alioongozana nao kwa lengo la kushiriki katika ziara ya kubadilishana uzoefu kati ya Tanzania na Msumbiji kuhusu hatua za mapema kabla ya majanga unaoendelea kwa siku tano kuanzia tarehe 25 hadi 29 Mei, 2026 Mjini Maputo Msumbiji.

Dkt. Yonazi amezungumza na watumishi wa ubalozi huo na kupokea taarifa fupi ya utekelezaji wa majukumu ya Ubalozi iliyotolewa na Mwambata fedha Bw. Samson Marwa kwa niaba ya Mhe. CP. Hamad Khamis Hamad, Balozi wa Tanzania nchini Msumbiji ambaye alikuwa katika majukumu mengine.

Aidha, amewashukuru watumishi wa ubalozi huo kwa namna wanavyoendelea kutekeleza majukumu ya msingi huku wakiiwakilisha nchi na kutekeleza diplomasia ya uchumi kwa vitendo.

“Ninawapongeza namna mnavyoendelea kuiwakilisha nchi yetu, ni vyema kuendelea kuangalia fursa zilizopo na kuzitangaza hususan za kiuchumi zitakazowavutia kuja kuwekeza Tanzania, niwasihi kuendelea kuwa mabalozi wazuri wa nchi yetu,” alisema Dkt. Yonazi

Kwa upande wake Mwambata fedha wa ubalozi huo Bw.Samson Marwa akizungumza kwa niaba ya Balozi wa Tanzania nchini Msumbiji alimshukuru Katibu Mkuu huyo kwa kutenga muda wake na kuzitembelea ofisi za ubalozi huku akiahidi kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi na kuhakikisha jukumu la msingi la kuhakikisha uhusiano kati ya Tanzania na Msumbiji linaendelea kuimarika kwa manufaa ya nchi hizo mbili.

“Tunashukuru kwa ziara hii muhimu kwetu, mnapotembelea ofisi zetu za ubalozi inaonesha kujali na kutambua kazi zinazofanywa, tunaahidi kuendeleza diplomasia na kuitangaza nchi yetu na fursa zilizopo Tanzania,” alisema Marwa

Sambamba na hilo alieleza dhamira ya kuimarisha ushirikiano wa kihistoria na wa kidugu kati ya Tanzania na Msumbiji huku akisisitiza umuhimu wa kuendeleza ushirikiano kati ya nchi hizo mbili kwa kuzingatia mchango wa Tanzania kwa Taifa hilo.








Na Janeth Raphael -MichuziTv Bungeni,Dodoma

Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki imeeleza kuwa vipaumbele vyake kwa mwaka wa fedha 2026/2027 vitaendelea kutekelezwa kwa kuzingatia miongozo ya kitaifa, kikanda na kimataifa inayolenga kuimarisha maendeleo endelevu na ushirikiano wa kimataifa.

Akizungumza Bungeni, leo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Dkt. Mahmoud Thabit Kombo (Mb.), amesema wizara hiyo itaongozwa na nyaraka mbalimbali za kimkakati zikiwemo Sera ya Mambo ya Nje ya mwaka 2001, toleo la mwaka 2024, pamoja na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Aidha, amesema utekelezaji wa vipaumbele hivyo pia utazingatia Dira ya Maendeleo ya Zanzibar 2050 pamoja na Mpango wa Nne wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano (2026/2027 – 2030/2031), ambao unalenga kuimarisha uchumi na ustawi wa wananchi kupitia sekta mbalimbali za maendeleo.

Kwa mujibu wa Waziri Kombo, mipango hiyo pia itaendana na Mpango wa Maendeleo wa Zanzibar (2021–2026) pamoja na Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025, ambayo imeweka malengo ya kimkakati ya maendeleo ya taifa katika kipindi kijacho.

Katika hatua nyingine, Wizara hiyo itaendelea kuzingatia mikataba ya kikanda na kimataifa ikiwemo Mkataba wa Jumuiya ya Afrika Mashariki wa mwaka 1999, Mkataba wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) wa mwaka 1992, pamoja na Ajenda ya Umoja wa Mataifa ya Maendeleo Endelevu 2030.

Vilevile, utekelezaji wa vipaumbele hivyo utaongozwa na Ajenda ya Umoja wa Afrika 2063, Dira ya SADC ya mwaka 2050 na Dira ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya mwaka 2050, sambamba na mikataba mingine ya kikanda na kimataifa inayolenga kuimarisha ushirikiano wa mataifa.

Waziri Kombo amebainisha kuwa Wizara pia itaendelea kuzingatia maelekezo ya viongozi wakuu wa kitaifa pamoja na ushauri unaotolewa na Bunge katika kuhakikisha sera na mikakati ya diplomasia ya nchi inatekelezwa kwa ufanisi.

Kwa mujibu wake, vipaumbele vya Wizara kwa mwaka wa fedha 2026/2027 vitajikita katika maeneo makuu manne, ambayo ni kuimarisha uratibu na ushirikiano wa nchi mbili, kikanda na kimataifa, pamoja na kusimamia utekelezaji wa Sera ya Mambo ya Nje ya mwaka 2001 (toleo la 2024), hususan katika eneo la diplomasia ya uchumi.

Maeneo mengine ni kulinda taswira, heshima na maslahi ya Taifa katika nyanja za kimataifa, pamoja na kuboresha mazingira ya utendaji kazi kwa watumishi wa Wizara, kuimarisha utawala bora, rasilimali watu na utekelezaji wa miradi ya maendeleo ndani ya Wizara na taasisi zake.

Hatua hiyo inalenga kuimarisha nafasi ya Tanzania katika majukwaa ya kimataifa sambamba na kukuza ushirikiano wa kiuchumi, kisiasa na kijamii kwa manufaa ya wananchi.







Top News