MTWARA – Serikali kupitia Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora imeipongeza Taasisi ya Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) kwa mchango wake mkubwa wa kupunguza watumishi wasio na maadili na kuongeza tija serikalini. Pongezi hizo zimetolewa leo, Juni 11, 2026, mkoani Mtwara na Naibu Katibu Mkuu wa ofisi hiyo, Bw. Xavier Mrope Daudi, wakati akifungua rasmi Baraza la Sita la Wafanyakazi wa chuo hicho.Akizungumza katika ufunguzi huo, Bw. Daudi alisema kuwa Serikali inatambua na kuthamini juhudi kubwa zinazofanywa na chuo hicho katika kuandaa watumishi wa umma kupitia mafunzo mbalimbali. Aliongeza kuwa matunda ya kazi nzuri ya chuo hicho yameleta matokeo chanya kwa kiasi kikubwa katika kuboresha utendaji kazi na nidhamu maeneo ya kazi, jambo linalochangia kuwepo kwa watumishi wenye tija na uadilifu mkubwa.


Aidha, Naibu Katibu Mkuu alisisitiza umuhimu wa kutoa huduma bora na kutumia lugha yenye staha kwa wateja, akibainisha kuwa chuo hicho ndicho jiko linalopika watumishi wa umma tangu wanapoingia hadi wanapotoka kazini, hivyo wanapaswa kuwa mfano wa kuigwa. Alitoa rai pia kwa uongozi wa chuo kuendelea kubuni mifumo mipya ya TEHAMA kwa kushirikiana na mamlaka husika ili kurahisisha utoaji wa mafunzo kwa watumishi na jamii kwa ujumla, hasa kwa kuwa chuo hicho tayari kiko mstari wa mbele katika matumizi ya teknolojia.

Kuhusu baraza hilo la wafanyakazi, Bw. Daudi alieleza kuwa ni chombo muhimu kinachotoa fursa ya kujadiliana masuala ya tija, ufanisi, na maslahi ya watumishi. Alihimiza uwepo wa maelewano, ushirikiano, na nidhamu kazini ili kuleta mshikamano utakaosaidia chuo kupiga hatua zaidi katika nyanja za mafunzo, tafiti, na ushauri wa kitaaluma, huku akitaka majadiliano ya baraza hilo yatawaliwe na hekima, busara, na uwazi.
Kwa upande wake, Mkuu wa Chuo na Mtendaji Mkuu wa TPSC, Dkt. Ernest Mabonesho, ameishukuru serikali kwa kukipatia chuo hicho jumla ya Shilingi bilioni 8.4 katika kipindi cha miaka mitatu kuanzia mwaka wa fedha 2024/25 hadi 2026/27. Fedha hizo zimetengwa kwa ajili ya ujenzi wa Kampasi ya Tanga, ambapo ujenzi wake unaendelea vizuri baada ya kupokea bilioni 1.5 katika awamu ya kwanza, bilioni 2.6 awamu ya pili, na bilioni 4.3 zilizotengwa kwa ajili ya mwaka mpya wa fedha unaoanza Julai 2026.

Dkt. Mabonesho alibainisha kuwa baraza hilo la sita linajumuisha wajumbe 64 kutoka kampasi zote sita za chuo hicho, wakiwemo wawakilishi wa menejimenti, wafanyakazi, na viongozi wa chama cha wafanyakazi (TUGHE). Katika kikao hicho cha Mtwara, wajumbe watapitia na kujadili Mpango Mkakati wa Miaka Mitano (2026/27 - 2030/31), Mpango wa Bajeti ya mwaka ujao wa fedha, pamoja na tathmini ya utekelezaji wa bajeti ya kipindi kilichopita ili kuweka vipaumbele thabiti.

Alihitimisha kwa kusisitiza kuwa wafanyakazi wote wa TPSC wamejipanga kufanya kazi kwa weledi, uadilifu, na bidii ili kutekeleza kwa ufanisi malengo ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, yenye kusudi la kuleta maendeleo na kuondoa umaskini nchini.






















 

Na Janeth Raphael MichuziTv 

Serikali imezindua rasmi mpango wa ukopeshaji wa majiko ya umeme kwa wateja wa TANESCO pamoja na mradi wa vituo vya kuchajia vyombo vya usafiri vinavyotumia umeme, hatua inayolenga kuhamasisha matumizi ya nishati safi, kupunguza gharama za maisha kwa wananchi na kuchochea ukuaji wa uchumi wa taifa.

Akizungumza katika hafla ya utiaji saini wa makubaliano ya utekelezaji wa mpango huo iliyofanyika jijini Dodoma, Waziri wa Nishati,  Deogratius Ndejembi (Mb.), alisema miradi hiyo ni sehemu ya matokeo ya uwekezaji mkubwa uliofanywa na Serikali katika sekta ya umeme na kwamba sasa wananchi wanaanza kunufaika moja kwa moja na maboresho hayo.

Amesema matumizi ya umeme katika kupikia na usafiri yatawezesha familia nyingi za Kitanzania kupunguza matumizi ya fedha kwa ajili ya nishati, kuongeza muda wa kufanya shughuli za maendeleo na kuboresha mazingira ya maisha kutokana na matumizi ya nishati safi.

Waziri Ndejembi ameeleza kuwa Serikali inaona matumizi ya umeme katika sekta hizo kama njia muhimu ya kuongeza matumizi yenye tija ya umeme unaozalishwa nchini, kuongeza mapato ya TANESCO, kuvutia uwekezaji mpya na kuimarisha shughuli za kiuchumi.

Aidha, alisema hatua hiyo itafungua fursa mbalimbali za kiuchumi kwa vijana, wanawake na sekta binafsi kupitia biashara za usambazaji wa vifaa vya nishati safi, huduma za teknolojia, matengenezo ya vifaa vinavyotumia umeme pamoja na uwekezaji katika miundombinu ya kuchajia vyombo vya usafiri vya umeme.

"Hii ndiyo Tanzania tunayoijenga, Tanzania inayotumia rasilimali zake kuleta maendeleo kwa wananchi wake na inayokwenda sambamba na mabadiliko ya teknolojia duniani," alisema Waziri Ndejembi.

Katika kuhakikisha mpango huo unaleta matokeo yaliyokusudiwa, Waziri huyo aliiagiza TANESCO kuhakikisha huduma ya mikopo ya majiko ya umeme inawafikia wananchi wengi zaidi katika maeneo yote ya nchi, mijini na vijijini, huku akisisitiza umuhimu wa kuongeza elimu kwa umma kuhusu faida za matumizi ya umeme katika kupikia na matumizi sahihi ya vifaa vinavyookoa nishati.

Pia alitaka vituo vya kuchajia vyombo vya usafiri vinavyotumia umeme vijengwe kwa wakati na kutoa huduma za uhakika kwa wananchi, huku ushirikiano kati ya TANESCO na sekta binafsi ukiendelea kuimarishwa ili kuongeza uwekezaji katika teknolojia za nishati safi.

Waziri Ndejembi aliwataka wananchi kuchangamkia fursa ya mikopo ya majiko ya umeme, akieleza kuwa masharti yaliyowekwa ni nafuu na rahisi kufikiwa na wengi. Alisema anayehitaji kunufaika na mpango huo anatakiwa kuwa mteja wa TANESCO, awe mmiliki wa nyumba anayenunua umeme mara kwa mara na awe na mita yenye taarifa zinazolingana na Kitambulisho cha Taifa (NIDA).

Katika hatua nyingine, alisema TANESCO itatoa huduma ya kuchaji vyombo vya usafiri vinavyotumia umeme bila malipo kwa siku 30 za mwanzo tangu kuanza kwa huduma hiyo ili kuwapa wananchi nafasi ya kuifahamu na kuitumia teknolojia hiyo mpya. Baada ya hapo, gharama zitakazotozwa zitakuwa nafuu na zinazoweza kumuduwa na wananchi wengi.

Kwa upande wa sekta binafsi, Waziri huyo alisisitiza kuwa Serikali itaendelea kuboresha mazingira ya uwekezaji katika teknolojia za nishati safi ili kuongeza ushiriki wa wawekezaji katika kuendeleza sekta ya nishati na kuharakisha safari ya Tanzania kuelekea matumizi makubwa ya nishati safi na uchumi wa kisasa.

Uzinduzi wa miradi hiyo unaashiria hatua mpya katika juhudi za Serikali za kuhamasisha matumizi ya umeme katika maisha ya kila siku ya Watanzania, huku ukitarajiwa kuongeza kasi ya matumizi ya nishati safi na kuchangia maendeleo endelevu ya kijamii na kiuchumi nchini.







Na Janeth Raphael MichuziTv - Bungeni Dodoma


Serikali imeendelea kuweka msukumo mkubwa katika kuhamasisha matumizi ya nishati safi na mbadala nchini, hususan umeme na gesi asilia, katika sekta ya usafiri na matumizi ya majumbani, kupitia mapendekezo mapya ya hatua za kodi kwa mwaka wa fedha 2026/27.

Akiwasilisha mapendekezo ya Serikali ya makadirio ya mapato na matumizi Bungeni, Waziri wa Fedha,Balozi Dkt Khamis Mussa Omar, amesema Serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali za kifedha na kodi zinazolenga kupunguza gharama za uwekezaji na kuongeza matumizi ya teknolojia rafiki kwa mazingira.

Kwa mujibu wa mapendekezo hayo, Serikali imeendelea kutoa msamaha wa ushuru wa bidhaa kwa magari yanayotumia umeme na gesi asilia kwa kuzingatia ukubwa wa injini, sambamba na msamaha wa Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) kwenye gesi asilia iliyoshindiliwa (CNG) inayotumika kwenye magari.

Aidha, Serikali imeondoa VAT kwenye vifaa vinavyotumika katika miundombinu ya gesi asilia (CNG), ikiwemo compressors, vifaa vya kupimia, mitambo ya kuhifadhi gesi, magari maalum ya usafirishaji na pampu za kujazia gesi. Hatua hiyo pia inahusisha msamaha wa kodi katika mnyororo mzima wa uzalishaji wa CNG pamoja na vifaa vinavyotumika kubadili magari kutoka mafuta ya petroli kwenda kwenye gesi au umeme.

Katika sekta ya uzalishaji wa ndani, Serikali imeweka pia msamaha wa VAT kwenye malighafi zinazotumika kutengeneza mitungi ya gesi kwa matumizi ya majumbani na magari, pamoja na kutoa unafuu wa ushuru wa forodha kwa waunganishaji na wazalishaji wa vyombo vya moto vinavyotumia nishati safi nchini chini ya kanuni za Jumuiya ya Afrika Mashariki za mwaka 2025.

Kwa mwaka wa fedha 2026/27, Serikali inapendekeza hatua zaidi ikiwemo msamaha wa VAT kwa vifaa vya vituo vya kuchaji magari ya umeme (EV charging stations), pamoja na kupunguza ushuru wa forodha kutoka asilimia 25 hadi asilimia 10 kwa magari yanayotumia umeme.

Pia, Serikali imependekeza msamaha wa VAT kwa mita janja za gesi ya kupikia (LPG smart meters) zitakazoingizwa nchini na kusambazwa na wasambazaji wa gesi pekee, sambamba na majadiliano ya kutoa unafuu wa kodi kwa waunganishaji wa magari ya umeme nchini ili kuchochea uzalishaji wa ndani.

Hatua hizo Serikali inasema, zinalenga kupunguza gharama za matumizi ya nishati safi, kuvutia uwekezaji katika sekta ya nishati mbadala, kuimarisha viwanda vya ndani, na hatimaye kulinda mazingira kupitia upunguzaji wa matumizi ya mafuta ya kisukuku.

Kwa ujumla, mkakati huu unaonekana kuwa sehemu ya mpango mpana wa Serikali wa kuhamia kwenye uchumi wa kijani unaotegemea nishati safi na endelevu nchini.


Na Pamela Mollel,Arusha 

Jitihada za kuhakikisha Watanzania wengi zaidi wanapata huduma za nishati safi ya kupikia zimepewa msukumo mpya baada ya wadau kutoka sekta ya umma, binafsi na mashirika ya maendeleo kukutana jijini Arusha kujadili mikakati ya kuharakisha upatikanaji wa nishati hiyo nchini. Mkutano huo umejadili fursa, changamoto na mbinu za kuongeza matumizi ya teknolojia za kupikia ambazo ni salama kwa afya na mazingira.

Akifungua mkutano huo, Naibu Waziri wa Nishati, Salome Makamba, alisema Tanzania imepata mafanikio makubwa katika utekelezaji wa ajenda ya nishati safi ya kupikia, ambapo kiwango cha matumizi kimeongezeka kutoka asilimia 6.9 mwaka 2021 hadi asilimia 28.6 mwaka 2025. Alisema ongezeko hilo linaonesha namna juhudi za Serikali na ushirikiano wa wadau mbalimbali zinavyoendelea kuleta matokeo chanya katika kuboresha maisha ya wananchi.

Makamba alibainisha kuwa Serikali imeweka lengo la kuhakikisha asilimia 80 ya Watanzania wanatumia nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034 kupitia utekelezaji wa Mkakati wa Taifa wa Nishati Safi ya Kupikia wa mwaka 2024–2034. Alisema mkakati huo umejikita katika kuongeza upatikanaji wa teknolojia nafuu za kupikia, kuimarisha ushiriki wa sekta binafsi na kuhamasisha wananchi kubadili matumizi ya nishati za jadi zinazochangia uharibifu wa mazingira.

Alieleza kuwa mafanikio yaliyofikiwa hadi sasa yamechangiwa na utekelezaji wa miradi mbalimbali ikiwemo usambazaji wa mitungi 452,445 ya gesi ya LPG, majiko banifu zaidi ya 200,000 pamoja na mradi wa CookFund unaofadhiliwa na Umoja wa Ulaya kupitia UNCDF. Miradi hiyo imewezesha mamia ya maelfu ya wananchi katika mikoa mbalimbali kupata huduma za nishati safi na salama ya kupikia.

Katika mkutano huo, Balozi wa Umoja wa Ulaya nchini Tanzania, Christine Grau, alitangaza kuwa EU imetenga euro milioni 30, sawa na zaidi ya shilingi bilioni 92, kwa ajili ya kusaidia upanuzi wa matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini. Alisema uwekezaji huo unalenga kuimarisha masoko ya nishati endelevu, kuvutia uwekezaji wa sekta binafsi na kuongeza upatikanaji wa huduma kwa wananchi wa maeneo ya mijini na vijijini.

Grau alisema ufadhili huo ni sehemu ya mkakati wa Global Gateway unaolenga kuharakisha maendeleo endelevu kupitia uwekezaji katika sekta muhimu za kiuchumi. Alisisitiza kuwa matumizi ya nishati safi ya kupikia yana mchango mkubwa katika kulinda mazingira, kupunguza ukataji wa miti na kuboresha afya za wanawake na watoto ambao mara nyingi huathiriwa na moshi unaotokana na matumizi ya nishati za jadi.

Kwa mujibu wa wadau walioshiriki mkutano huo, ushirikiano kati ya Serikali, washirika wa maendeleo na sekta binafsi utaendelea kuwa nguzo muhimu katika kufanikisha ajenda ya nishati safi ya kupikia nchini. Walisema hatua zinazochukuliwa kwa sasa zinaipa Tanzania nafasi nzuri ya kufikia malengo yake ya mwaka 2034 huku zikichangia ustawi wa wananchi, uhifadhi wa mazingira na maendeleo ya uchumi wa taifa kwa ujumla.






Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, akiwa katika picha ya pamoja na Bw. Massad Boulos, mwanadiplomasia na Mshauri Mwandamizi wa Rais Donald Trump kuhusu masuala ya Afrika, nchi za Kiarabu na Mashariki ya Kati, baada ya kufanya mazungumzo pembezoni mwa Mkutano wa Oslo Forum unaofanyika Oslo, Norway.


Mkutano huo, unaofanyika kuanzia tarehe 10 hadi 12 Juni, 2026, umewakutanisha viongozi, wanadiplomasia waandamizi na wadau wa masuala ya amani, diplomasia na usuluhishi kutoka nchi mbalimbali zenye ushawishi duniani.

Kamishna wa Uhifadhi TANAPA, CPA Musa Nassoro Kuji amekabidhi kwa Bodi ya Wadhamini ya TANAPA Tuzo ya Mafanikio katika Utoaji wa Huduma bora Mwaka 2026 (Quality Achievement Award 2026) pamoja na Cheti cha Ushindi wa Pili (First Runner-Up) katika Tuzo za Ubora wa Taifa 2025/2026 kwenye kikao cha bodi hiyo kinachoendelea leo Juni 11, 2026 jijini Dar es salaam.

Tuzo ya “Quality Achievement Award 2026” ilitolewa tarehe 31 Mei 2026 jijini Brussels, Ubelgiji na Taasisi ya “European Society for Quality Research (ESQR)” huku Cheti cha Ushindi katika Tuzo za Ubora wa Taifa 2025/2026 kilitolewa na Shirika la Viwango Tanzania kwa kutambua taasisi zinazofanya vizuri katika utoaji wa huduma na kuzingatia viwango vya ubora, kilitolewa juni 05, 2026 jijini Dar es salaam.

Bodi ya Wadhamini TANAPA inayoongozwa na Mwenyekiti wake  Jenerali George Waitara, Mkuu wa Majeshi Mstaafu, imepokea tuzo hizo na kuipongeza Menejimenti ya Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania, Maafisa na Askari Uhifadhi kwa kuendelea kutambulika kimataifa na kitaifa katika kusimamia utekelezaji wa majukumu ya TANAPA ya uhifadhi na maendeleo ya utalii nchini. 

Vilevile, Bodi ya Wadhamini imetoa wito kwa watumishi wote wa Shirika kuhakikisha kuwa kila mmoja anatimiza wajibu wake kikamilifu ili kuendelea kufanikisha malengo ya Shirika na Taifa kwa ujumla pamoja na kupata tuzo nyingi zaidi.










London, Juni 10, 2026: Airtel Africa Plc (“Airtel Africa”), 
KAMPUNI inayoongoza katika utoaji wa huduma za mawasiliano na huduma za kifedha kwa njia ya simu katika nchi 14 barani Afrika ikiwemo Tanzania, imechapisha Ripoti yake ya Maendeleo ya 2026, inayobainisha mafanikio yaliyopatikana katika kupanua huduma za mawasiliano, kuimarisha ujumuishi wa kifedha na kuchochea maendeleo endelevu katika jamii inazohudumia kwa kipindi cha mwaka wa fedha 2025/26.

Ripoti hiyo inaonesha jinsi uwekezaji wa Airtel Africa katika miundombinu ya kidijitali, huduma za kifedha kupitia simu za mkononi, pamoja na ushirikiano wa kimkakati, ulivyoendelea kubadilisha maisha ya watu na kufungua fursa za kiuchumi na kijamii kwa jamii ambazo bado hazijafikiwa kikamilifu na huduma hizo, hususan katika nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara.

Aidha, ripoti hiyo inaeleza hatua mbalimbali zinazoendelea kuchukuliwa na Airtel Africa katika matumizi ya nishati mbadala, pamoja na mbinu zake za kuendesha biashara kwa kuzingatia uwajibikaji, uhifadhi wa mazingira na uwazi katika utoaji wa taarifa za maendeleo kwa wadau wake.

Akizungumzia ripoti hiyo, Mtendaji Mkuu wa Airtel Africa, Sunil Taldar, alisema:

"Barani Afrika, upatikanaji wa mawasiliano, huduma za kifedha na elimu ya kidijitali unazidi kuwa muhimu katika kufungua fursa za kiuchumi. Airtel Africa inaendelea kupanua huduma hizi kwa mamilioni ya watu, hususan katika maeneo ya vijijini na yale ambayo bado hayajafikiwa kikamilifu."

“Katika mwaka huu, tumeendelea kupanua huduma za mtandao, kuongeza matumizi ya simu janja na kuimarisha huduma za Airtel Money, sambamba na kuendeleza ushirikiano wa kimkakati unaochangia mafanikio ya shughuli zetu. Maendeleo haya yameendelea kuwa sehemu muhimu ya mkakati wetu wa kukuza biashara na kutoa huduma bora kwa wateja. Aidha, kwa kuboresha matumizi ya nishati na kupunguza utegemezi wa dizeli, tunaimarisha ufanisi na ustahimilivu wa shughuli zetu, huku tukichangia ukuaji endelevu wa biashara na jamii.”

Vigezo muhimu vya Mazingira, Jamii na Utawala Bora (ESG) kwa Mwaka 2025/26

1. Kupanua Mawasiliano na Kupunguza Pengo la Kidijitali

● Watu wanaofikiwa na mtandao wa simu umefikia asilimia 81.9, kutoka asilimia 81.2 mwaka 2024/25.

● Upatikanaji wa huduma za mtandao katika maeneo ya vijijini umeongezeka hadi asilimia 73.1, kutoka asilimia 72.2 mwaka uliotangulia.

● Idadi ya wateja wanaotumia huduma za data umeongezeka hadi asilimia 45.9, kutoka asilimia 44.2.

● Matumizi ya simu janja yaliongezeka hadi asilimia 49.5, kutoka asilimia 44.8, hatua inayowezesha watu wengi zaidi kupata huduma za mtandao na majukwaa ya kidijitali.

● Thamani ya miamala iliyofanyika kupitia programu ya My Airtel imefikia dola za Marekani bilioni 8.3, ikiwa ni ongezeko la asilimia 80 ikilinganishwa na mwaka uliopita, huku watumiaji hai wa kila mwezi wakifikia milioni 10.5.

2. Kuimarisha Ujumuishaji wa Kifedha na Ushiriki wa Kiuchumi

● Idadi ya wateja wa Airtel Money imeongezeka na kufikia zaidi ya milioni 54, kutoka milioni 44.6 mwaka 2024/25.

● Asilimia 44.1 ya wateja wa Airtel Money ni wanawake.

● Thamani ya miamala iliyochakatwa kupitia Airtel Money ni takribani dola za Marekani bilioni 196, kutoka dola bilioni 136 mwaka uliopita.

3. Kusaidia Elimu, Ujuzi na Fursa za Ajira

● Mtandao wa mawakala wa Airtel Money uliongezeka na kufikia mawakala milioni 2.4, kutoka milioni 1.7 mwaka 2024/25, hatua inayochangia ujasiriamali, ajira na upatikanaji wa huduma za kifedha.

● Uwiano wa wanawake katika nguvu kazi ya Airtel Africa uliongezeka hadi asilimia 29.9, kutoka asilimia 29.2 mwaka uliopita.

● Kufikia Machi 31, 2026, jumla ya shule 3,043 zilikuwa zimeunganishwa na huduma za intaneti bila malipo kupitia ushirikiano kati ya Airtel Africa Foundation na UNICEF, kutoka shule 2,176 mwaka 2024/25.

4. Kupunguza Athari za Mazingira Zinazotokana na Shughuli za Kampuni

● Zaidi ya maeneo 950 ya miundombinu ya kampuni yalibadilishwa kutoka matumizi ya nishati isiyounganishwa na gridi ya taifa kwenda kwenye umeme wa gridi ya taifa, kutoka maeneo 500 mwaka uliopita.

● Matumizi ya dizeli yalipunguzwa kwa lita milioni 9.1 katika kipindi cha mwaka mmoja.

● Asilimia 94 ya taka zote zilizozalishwa zilirejelewa (recycled), ikilinganishwa na asilimia 93 mwaka 2024/25.

Ripoti ya Maendeleo ya 2026 imeandaliwa kwa kuzingatia viwango vya kimataifa vya Global Reporting Initiative (GRI) pamoja na miongozo ya sekta ya mawasiliano ya simu ya GSMA.
Kuhusu Airtel Africa

Airtel Africa ni mtoa huduma wa mawasiliano na huduma za fedha kwa njia ya simu anayehudumia zaidi ya wateja milioni 183.5 katika nchi 14 za Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara. Kampuni inalenga kuendeleza ujumuishi wa kidijitali na kifedha kwa kuwafungulia wananchi fursa za maendeleo na kuboresha maisha yao kupitia huduma za mawasiliano na teknolojia.

Mdhibiti Ubora Mkuu wa NACTVET Nicholaus Moshi akizungumza na Waandishi wa habari kuhusiana na Shindano la Ubunifu wa Ushonaji wa Mavazi kwa Kanda ya Dar es Salaam lililofanyika Chuo cha Anna Academy.Mkurugenzi wa Chuo cha Anna Academy Anna Lunguya akizungumza kuhusiana mashindano hayo katika ubunifu wakiwa ndio watarajiwa wa kuiwakilisha nchi kudunia katika mashindano baada ya kufanyika mchujo wa kitaifa.

Washiriki Tisa wakijiandaa katika shindano la ubunifu wa Ushonaji wa  mavazi.

Picha katika Makundi mbalimbali wakati wa maandalizi ya Shindano la Ubunifu wa Ushonaji Mavazi lililofanyika katika Chuo cha Anna Academy.

Na Chalila Kibuda, Michuzi TV
NCHI  ya Tanzania kushiriki mashindano ya ubunifu na ubobezi wa katika Fani Tisa kwa kushirikisha wanafunzi wa Vyuo vya Ufundi Stadi ambapo washindi wataopatikana katika Kanda wataingia ngazi Kitaifa watachunjwa kujiandaa kuwakilisha nchi kidunia.

Mkurugenzi wa Udhibiti Ubora wa NACTVET Joffrey Oleke amesema mashindano yalianza katika ngazi ya vyuo ambao washindi wanaingia katika mashindano ya kikanda.

Mashindano katika Fani ya ubunifu wa Ushonaji wa Mavazi Kanda ya Dar es Salaam yamefanyika katika Chuo cha Anna Academy kwa washiriki Tisa katika fani hiyo ambapo Katika mchujo watabaki wa tano ambao wataingia katika mashindano ya Kitaifa yatayofanyika mkoani Tanga Agasti Mwaka huu.

Akizungumza kwenye Mashindano Ubunifu wa Ushonaji wa Mavazi Mdhibiti Ubora Mkuu wa NACTVET Kanda ya Mashariki, Nicholaus Moshi, amesema mashindano hayo ni jukwaa muhimu la kuibua vipaji, kukuza ubunifu na kuandaa vijana watakaoiwakilisha Tanzania katika mashindano ya ngazi za kikanda na kimataifa.

Washiriki Tisa wanatoka maeneo mbalimbali ambao wanapimwa uwezo wao katika ubunifu, ukataji na ushonaji wa mavazi kwa kutumia viwango vya kimataifa.

Amesema washiriki hao wanatarajiwa kuchujwa ili kupata washindi watakaowakilisha Tanzania katika hatua zinazofuata za mashindano ya ujuzi ngazi ya kikanda na kimataifa.

“Mashindano haya yanalenga kupima uwezo wa vijana wetu katika ubunifu, ushonaji na matumizi ya teknolojia ya kisasa katika sekta ya mavazi. Tunafurahi kuona vijana wameandaliwa vizuri kisaikolojia, kitaaluma na kwa vitendo ili kuonyesha uwezo wao,” amesema Moshi.

Ameongeza kuwa vifaa vinavyotumika katika mashindano hayo ni vya kisasa na vinavyotumika katika tasnia ya ubunifu na ushonaji duniani kote, jambo linalowawezesha washiriki kupata uzoefu unaokidhi viwango vya kimataifa.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Ana Collection Academy, Anna Lunguya, amesema taasisi hiyo inajivunia kuwa mwenyeji wa mashindano hayo ambayo yana mchango mkubwa katika kukuza sekta ya ubunifu na ushonaji nchini.

Amesema sekta ya ubunifu na ushonaji imekuwa chanzo muhimu cha ajira na biashara kwa vijana wengi, hivyo mashindano hayo yatasaidia kuibua vipaji vipya na kupata wabunifu watakaoweza kuiwakilisha Tanzania katika ngazi mbalimbali za Afrika na duniani.

Na Hassan Kimweri, WAF – Tabora.

Jumla ya macho 996 yamefanyiwa uchunguzi kwa wagonjwa 823 wanaotarajiwa kufanyiwa upasuaji wa mtoto wa jicho katika kambi maalum ya madaktari bigwa iliyowekwa na Serikali kwa kushirikiana na Taasisi ya 'Helen Keller International' na wadau wengine wa sekta ya afya.  

Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Igunga Mhe. Elizabeth Rwegasila amesema hayo leo wakati wa ufunguzi wa kambi ya madaktari bingwa wa macho iliyowekwa katika Hospitali ya Wilaya ya Igunga mkoani Tabora ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuboresha afya ya macho na kuondoa tatizo la upofu kwa wananchi. 

"Idadi hii inaonesha ukubwa wa mahitaji ya huduma za macho kwa wananchi wa eneo hili, wanaonufaika na huduma hiyo wanapatiwa huduma mbalimbali muhimu ikiwemo usafiri kutoka majumbani mwao, malazi, chakula pamoja na huduma za matibabu kabla na baada ya upasuaji," amesema Mhe. Rwegasila

Aidha, amelishukuru Shirika la Helen Keller International kwa kuendelea kushirikiana na Serikali katika kuboresha huduma za afya ya macho, akieleza kuwa mbali na kutoa huduma za matibabu, shirika hilo limechangia kuwajengea uwezo wataalamu wa afya ili kuendeleza huduma hizo hata baada ya mradi kukamilika.

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Wizara ya Afya Dkt. Greater Mande amesema mtoto wa jicho ni miongoni mwa sababu zinazosababisha upofu kwa wananchi wengi, kupitia kambi hiyo wagonjwa wengi wamepata fursa ya kurejeshewa uwezo wao wa kuona na kuendelea na shughuli zao za kila siku.

Pia, Dkt. Mande amewahimiza wananchi watakaonufaika na huduma hizo kuwa mabalozi kwa jamii zao kwa kutoa taarifa kwa watu wengine wenye changamoto za macho ili waweze kujitokeza kupata matibabu wanapopata fursa hiyo.

Nae, Mganga Mkuu wa Mkoa wa Tabora Dkt. Boniface Marwa amesema wataendelea kushirikiana na wadau ili huduma hiyo ya upasuaji na mtoto wa jicho inakua endelevu na wananchi waendelee kupata huduma hizo pamoja na kuwashukuru Helen Keller kwa kuwasimesha wataalam wa eneo hilo. 

Sambamba na hilo, Mkurugenzi wa Shirika ka Helen Keller International Dkt. Geogle kabona amesema msaada huo utaendelea kutolewa pamoja na kutoa huduma ya mafunzo kwa wataalamu wa eneo hilo pamoja na kutolewa kwa elimu ili jamii ipate uelewa huo. 

"Tutaendelea kushirikiana na Serikali katika juhudi za kupunguza upofu unaozuilika na kuhakikisha wananchi wengiz zaidi wanaoata huduma bira za afya ya macho," amesema Dkt. Kabona.








Top News