Rais wa Jamhuri ya Rwanda, Mhe. Paul Kagame amewasili nchini kwa Ziara ya Kikazi ya siku moja yenye lengo la kuimarisha uhusiano wa uwili kati ya Tanzania na Rwanda.

Mhe. Rais Kagame anatarajia kukutana na kufanya mazungumzo  na mwenyeji wake, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Ikulu jijini Dar es Salaam.

Inategemewa kwamba Ziara hii itadumisha mahusiano mazuri na ya kihistoria kati ya majirani hawa wawili. Ushirikiano huu umezidi kuimarika katika miaka ya hivi karibuni kwa kupitia Tume ya Kudumu ya Pamoja (JPC), ambapo Tanzania imeendelea kuwa miongoni mwa washirika wakuu watatu wa biashara wa Rwanda duniani, huku kiwango cha biashara kati ya nchi hizi kikiongezeka kila mwaka. 

Aidha, katika uwekezaji, kuanzia mwaka 1990 hadi Machi 2026, Tanzania imesajili miradi 42 ya uwekezaji kutoka Rwanda yenye thamani ya dola za Marekani milioni 325.53 na kuunda ajira 2,225 katika sekta mbalimbali ikiwemo viwanda, usafirishaji, huduma za kifedha, maliasili na utalii. 

Vilevile, wawekezaji wa Tanzania pia wamewekeza nchini Rwanda kupitia kampuni mbalimbali zikiwemo Bakhresa Group, Magodoro Dodoma, Discount Center, Jambo Plastic, Sagar Enterprises, Buffalo Travelling Tours, Maxcom Africa, Gasabo Grain Milling Company, LCM Delta Company na Metrex Integrated Consultancy.















▪️︎ Asema dini ni nguzo muhimu ya malezi na mshikamano wa Taifa

▪️︎ Asisitiza jamii kuendelea kuombea na kulinda amani ya nchi

Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba, amesema Serikali itaendelea kushirikiana kwa karibu na taasisi za dini nchini ili kuimarisha maadili, mshikamano wa kijamii na kudumisha amani ambayo ni msingi wa maendeleo endelevu ya Taifa.

Amesema hayo leo Jumapili, Mei 3, 2026, aliposhiriki ibada katika Kanisa Kuu la Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Mufindi, lililopo Mafinga Mjini, mkoani Iringa.

Akizungumza na waumini, Dkt. Nchemba amesema taasisi za dini zina mchango mkubwa katika kujenga jamii yenye maadili mema, inayozingatia misingi ya haki na uwajibikaji.

“Serikali inaendelea kusisitiza Watanzania wote kuwa wadau wa kuombea na kusimamia amani ya nchi yetu,” amesema.

Ameongeza kuwa mafanikio ya mipango ya maendeleo ya Taifa yanategemea uwepo wa amani.“Pasipokuwa na amani, hata malengo binafsi ya mtu mmoja mmoja ya Mtanzania mmoja mmoja hayawezi kufikiwa,” amesema.

Waziri Mkuu pia ameeleza mabadiliko ya mazingira ya dunia na changamoto zinazoweza kujitokeza.“Kuna aina mpya ya mapambano, na mapambano hayo ni ya rasilimali na kila palipo na rasilimali mara nyingi huwa kunavutia maadui na hupenda kupitia migawanyiko ya raia wa nchi hizo husika,” amesema.

Katika hatua nyingine, amepongeza juhudi za Kanisa katika malezi ya watoto na vijana.

“Maandalizi ya watoto hivi si tu manufaa kwa Kanisa, ni manufaa pia kwa Taifa tunalolitaka,” amesema.

Kwa upande wake, Askofu wa KKKT Dayosisi ya Mufindi, Dkt. Anthony Kipangula, ameipongeza Serikali kwa kazi ya kuwahudumia wananchi na kusisitiza kuwa ziara za Waziri Mkuu zimeonesha uongozi unaowagusa wananchi moja kwa moja.

“Nimeona juhudi zinazofanywa na Serikali katika kuwajali wananchi mtu wa ngazi yako kushuka mpaka kusikiliza kesi ya mwananchi na kumruhusu ajieleze, niliona ni maajabu kabisa,” amesema.

Ameongeza kuwa Kanisa litaendelea kushirikiana na Serikali katika kuhamasisha maadili mema, kutoa ushauri na kuliombea Taifa ili kudumisha amani na ustawi wa jamii.












Kampuni ya huduma za fedha kidigitali, Mixx, imeendelea kudhihirisha dhamira yake ya kuimarisha uchumi wa wakulima wa karafuu Zanzibar kwa kukabidhi hundi mbili zenye jumla ya shilingi milioni 175 kwa Shirika la Taifa la Biashara Zanzibar (ZSTC).

Akizungumza katika hafla hiyo, Mkuu wa Wilaya ya Mkoani-Pemba, Mhe. Mizza Hassan Faki alisema hatua hiyo ni sehemu ya juhudi endelevu za kampuni katika kuboresha maisha ya wakulima na kuleta mapinduzi katika sekta ya kilimo kupitia suluhisho za kifedha za kidigitali.

Katika makabidhiano hayo, Mixx ilikabidhi hundi ya shilingi milioni 150 kwa ajili ya kugharamia bima ya afya kwa wakulima wa zao la karafuu, hatua inayokamilisha ahadi ya jumla ya shilingi milioni 350 kutoka Mixx kwenda ZSTC. Aidha, hundi nyingine ya shilingi milioni 25 ilitolewa kwa ajili ya ununuzi wa miche 25,000 ya karafuu, ikiwa ni mkakati wa kuendeleza zao hilo muhimu kwa uchumi wa Zanzibar na Tanzania kwa ujumla. Vilevile, hafla hiyo ilishuhudia zoezi la upandaji wa miche ya karafuu, ikiwa ni ishara na dhamira ya pamoja katika kukuza na kulinda zao hilo.

Akielezea umuhimu wa ushirikiano huo, Afisa Mtendaji Mkuu wa Mixx, Bi. Angelica Pesha alisisitiza kuwa ushirikiano wa kimkakati kati ya Mixx na ZSTC umejengwa katika msingi wa kuhakikisha wakulima wanapata huduma bora za kifedha zinazowawezesha kuongeza tija na kipato chao. Alibainisha kuwa kupitia mfumo wa malipo kidigitali wa Mixx, kumekuwa na uwazi, upungufu wa upotevu wa fedha, na kuimarika kwa imani ya wakulima kwa taasisi zinazosimamia sekta hiyo.

“Tunaamini kuwa teknolojia ya kifedha ina nafasi kubwa katika kubadilisha maisha ya wakulima. Kupitia Mixx, tumefanikisha malipo ya haraka, salama na yenye uwazi, na kuondoa changamoto za ucheleweshaji wa malipo zilizokuwepo hapo awali,” alisema.

Kwa mujibu wa takwimu zilizotolewa, katika msimu wa karafuu wa 2025/2026, Mixx kwa kushirikiana na ZSTC imefanikiwa kufanya malipo ya zaidi ya shilingi bilioni 48 kwa wakulima wa Zanzibar. Hatua hiyo pia imechangia kuongezeka kwa ajira, ambapo zaidi ya mawakala 11,000 wamepata ajira na kushiriki katika mnyororo wa utoaji huduma za kifedha.

Aidha, Mixx ilitangaza mipango ya kuanzisha huduma ya mikopo nafuu kwa wakulima wa karafuu, inayotarajiwa kuanza kabla ya msimu wa 2026/2027, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuwawezesha wakulima kuwekeza zaidi katika uzalishaji.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa ZSTC, Ndugu Soud Said Ali, alieleza kuwa ushirikiano na Mixx umeleta mageuzi makubwa katika mfumo wa malipo kwa wakulima, na kuongeza ufanisi katika usimamizi wa zao la karafuu.

Mixx imeendelea kuahidi kushirikiana kwa karibu na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, ZSTC pamoja na wadau wengine ili kuhakikisha sekta ya karafuu inakuwa ya kisasa, yenye tija na endelevu kwa manufaa ya wakulima na uchumi wa Zanzibar kwa ujumla.










 

Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania (TCDC) imemtangaza Irene Luoga, Afisa Ushirika Mwandamizi kutoka Ofisi ya Mrajis Msaidizi wa Vyama vya Ushirika mkoa wa Mbeya, kuwa mfanyakazi hodari kwa mwaka 2025/2026.

Tuzo hiyo imetolewa kufuatia mchango wake mkubwa katika kusimamia na kuendeleza shughuli za ushirika, ikiwa ni pamoja na kuhamasisha uwajibikaji, uwazi na ufanisi katika Sekta ya ushirika.

Katika kipindi hicho, Irene ameonyesha weledi wa hali ya juu katika utekelezaji wa majukumu yake, akisimamia vyema shughuli mbalimbali za maendeleo ya Ushirika na kutoa msaada wa kitaalamu kwa wanachama na viongozi wa vyama. Juhudi zake zimechangia kuimarika kwa utendaji wa vyama vingi pamoja na kuongeza imani ya wanachama katika sekta ya ushirika nchini.

Akizungumza mara baada ya kupokea tuzo hiyo, Irene alieleza shukrani zake kwa Uongozi wa TCDC kwa kutambua mchango wake, akiahidi kuendelea kufanya kazi kwa bidii zaidi.

 “Ninawashukuru sana TCDC kwa kunichagua kuwa mfanyakazi hodari wa mwaka huu.Hii ni heshima kubwa kwangu na inanipa motisha ya kuendelea kufanya kazi kwa bidii, uadilifu na ufanisi zaidi ili kuleta maendeleo chanya katika sekta ya ushirika nchini na Taifa kwa ujumla,” alisema Irene.

 

Na Nasra Ismail, Geita

Mbunge wa Jimbo la Bukombe, Dkt. Doto Biteko, amemwagia sifa Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa (MNEC) Mkoa wa Geita, Gervas Evarist, akimtaja kama mhimili muhimu katika kuimarisha chama mkoani humo kupitia uboreshaji wa miundombinu.

Akizungumza kwenye mikutano ya shukrani kufuatia ushindi wa CCM katika Uchaguzi Mkuu wa 2025, Dkt. Biteko alibainisha kuwa mchango wa kifedha wa MNEC Evarist umewezesha ujenzi wa ofisi za kisasa katika kata mbalimbali, hususan wilayani Bukombe. 

Alieleza kuwa hatua hiyo ni kielelezo cha uongozi unaojali hadhi ya chama.Katika ziara hiyo iliyopita kwenye kata za Bulega, Bugelenga, Iyogelo, na Ng’anzo, Dkt. Biteko aliambatana na Mwenyekiti wa CCM Wilaya, Matondo Lutondo, ambapo alijionea miradi mbalimbali ikiwemo majengo ya biashara na nyumba za kulala wageni zinazomilikiwa na chama.

"Viongozi wanapimwa kwa kazi na si maneno. Uwepo wa ofisi bora na miradi ya kiuchumi ni siri ya utulivu na mafanikio ya chama chetu katika ngazi ya kata," alisisitiza Dkt. Biteko.

Mbali na masuala ya chama, Dkt. Biteko aliahidi kutoa mabati kwa ajili ya Zahanati ya Mtinga, huku Mwenyekiti wa Halmashauri, Erick Kagoma, akiwahimiza wananchi kuchangamkia mikopo ya 10% ya halmashauri ili kujiletea maendeleo.







Kiongozi wa Mbio za mwenge wa Uhuru kitaifa mwaka 2026 Wazo Mwang'onda ameridhishwa na kasi ya ujenzi wa mradi wa barabara ya Bohari yenye urefu wa mita 600 inayojengwa kwa kiwango cha lami katika mtaa wa Bohari Kata ya Mwenge Manispaa ya Lindi wenye thamani ya zaidi ya milioni 466

Akizungumza mara baada ya kuweka jiwe la msingi Leo Mei 2, 2026 Mwang'onda amewapongeza Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini TARURA kwa usimamizi mzuri wa Mradi huo ambao utachochea shughuli za kiuchumi kwa wananchi wa eneo hilo.

Awali akisoma taarifa mbele ya kiongozi huyo wa mbio za mwenge wa Uhuru mwaka 2026 Meneja wa TARURA Wilaya ya Lindi Mhandisi Downson Paschal amesema Mradi huo unaotekelezwa kwa fedha za Mfuko wa Mafuta   utekelezaji wake umefikia asilimia 90.

Amesema mkandarasi anayetekeleza mradi huo ni kampuni ya SEC ya Mtwara, ambapo ujenzi ulianza Septemba 20, 2024 na unatarajiwa kukamilika Mei 28, 2026 ukiwa na lengo la kuboresha miundombinu ya usafiri na kuchochea shughuli za kiuchumi kwa wananchi wa eneo hilo.

Ameongeza  kuwa hadi sasa kazi mbalimbali zimekwisha fanyika ikiwemo kusafisha eneo la barabara, kujenga tabaka la msingi pamoja na uwekaji wa mifereji na makalavati ili kuhakikisha barabara hiyo inadumu kwa muda mrefu.

Aidha amebainisha  kuwa kukamilika kwa mradi huo kutasaidia kurahisisha usafiri na usafirishaji wa bidhaa, kupunguza changamoto ya vumbi pamoja na kuongeza kasi ya maendeleo ya kiuchumi kwa wakazi wa Kata ya Mwenge wa Uhuru na maeneo jirani.

Baadhi ya wananchi wa Manispaa hiyo ya Lindi wameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutoa fedha za maendeleo ya miundombinu,  huku wakibainisha kuwa hatua hiyo imesaidia kuboresha huduma za kijamii na kiuchumi kwa wananchi.











Farida Mangube, Morogoro
CHUO Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kimesisitiza kuwa mafanikio yake katika tafiti, ufundishaji na utoaji wa huduma kwa jamii yanategemea kwa kiasi kikubwa mchango wa wafanyakazi wake, huku kikiahidi kuendelea kuboresha mazingira ya kazi ili kuongeza tija na ustawi kazini.

Akizungumza katika maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani (Mei Mosi), kwa niaba ya Makamu Mkuu wa Chuo, Prof. Raphael Chibunda, Naibu Makamu Mkuu wa Chuo upande wa Mipango, Fedha na Utawala, Prof. Amandus Muhairwa, amesema uongozi wa Chuo umejipanga kushughulikia changamoto mbalimbali zinazowakabili wafanyakazi na kuimarisha mazingira rafiki ya utendaji kazi.

Akijibu risala ya wafanyakazi, Prof. Muhairwa alieleza kuwa Menejimenti imepokea kwa uzito maoni, changamoto na mapendekezo yaliyowasilishwa, na itaendelea kuyafanyia kazi kupitia mifumo rasmi ya uongozi kwa lengo la kupata suluhisho endelevu.

Alibainisha kuwa SUA inaendelea kuboresha upatikanaji wa vitendea kazi kwa kuimarisha mifumo ya manunuzi na kushirikiana na wazabuni wenye uwezo wa kutoa huduma kwa wakati na kwa viwango vinavyokidhi mahitaji ya taasisi.

Aidha, alikiri kuwepo kwa changamoto ya uhaba wa ofisi, akieleza kuwa hali hiyo imetokana na ongezeko la watumishi ambapo jumla ya wafanyakazi 263 wameajiriwa katika kipindi cha miaka sita iliyopita, huku 125 wakistaafu, hali iliyoongeza shinikizo la miundombinu ya ofisi.

Prof. Muhairwa alisisitiza umuhimu wa kuendeleza ushirikiano, uwajibikaji na maadili kazini, akihimiza utamaduni wa kuheshimiana miongoni mwa wafanyakazi kwa kauli mbiu: “Mkubwa amheshimu mdogo na mdogo amheshimu mkubwa.”

Awali, Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi wa RAAWU tawi la SUA, Bw. Faraja Kamendu, pamoja na Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi THTU tawi la SUA, Dkt. Nickson Mkiramweni, waliwasilisha risala ya wafanyakazi wakieleza changamoto mbalimbali zinazowakabili, huku wakisisitiza umuhimu wa mshikamano, heshima na ushirikiano kazini.

Viongozi hao walieleza kuwa wana imani na utayari wa Menejimenti katika kushughulikia hoja zilizowasilishwa, na kuwahimiza wafanyakazi kujiunga na vyama vya wafanyakazi ili kulinda haki na maslahi yao kwa ufanisi zaidi.





Top News