📍Geita.

Mwenyekiti wa Kamati ya TEITI, Balozi Wilson Masilingi, ametembelea Mgodi wa Dhahabu wa Geita Gold Mining Limited akiambatana na Menejimenti ya TEITI, kwa lengo la kujitambulisha na kufanya mazungumzo na menejimenti ya mgodi huo.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Balozi Masilingi alisema ziara hiyo imelenga kujenga na kuimarisha ushirikiano kati ya TEITI na wadau wa sekta ya uziduaji, hususan migodi mikubwa inayochangia maendeleo ya taifa.

Alisema kuwa aliteuliwa kusimamia taasisi hiyo muhimu na Mhe.Dkt.Samia Suluhu Hassan, Rais wa Tanzania, mwezi Januari mwaka huu, hivyo anaona ni muhimu kujitambulisha kwa wadau wakuu wa sekta hiyo ili kuimarisha ushirikiano katika utekelezaji wa majukumu ya TEITI.

“Utekelezaji wa shughuli za EITI nchini ni wa ushirikiano, hivyo nitashirikiana kikamilifu na wadau wote ili kuendeleza gurudumu la uwazi na uwajibikaji katika sekta ya uziduaji,” alisema Balozi Masilingi.

Katika ziara hiyo, menejimenti ya mgodi ilitoa maelezo kuhusu maendeleo yaliyofikiwa tangu kuanzishwa kwa mgodi huo, ikiwemo namna wanavyotekeleza sheria, kanuni na miongozo ya sekta ya madini pamoja na masharti ya leseni ya uchimbaji.

Aidha, ilielezwa kuwa mgodi huo umeendelea kutenga fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya Uwajibikaji kwa Jamii (CSR) katika halmashauri mbalimbali za Mkoa wa Geita, hatua inayochangia maendeleo ya jamii zinazouzunguka mgodi.

Pia ilibainishwa kuwa kwa sasa mgodi huo unaendeshwa kwa kiasi kikubwa na Watanzania na umeendelea kuongeza ajira kwa wananchi wa ndani ikilinganishwa na miaka ya awali ya uendeshaji wake.

Balozi Masilingi aliishukuru menejimenti ya mgodi kwa mapokezi mazuri waliompatia pamoja na utayari wao wa kuendeleza ushirikiano kwa manufaa ya sekta ya uziduaji na maendeleo ya taifa.

Kwa upande wake, Katibu Mtendaji wa TEITI, Bi. Mariam Mgaya, aliishukuru menejimenti ya mgodi kwa kuendelea kushirikiana na TEITI katika utekelezaji wa matakwa ya EITI pamoja na Sheria ya TEITA ya mwaka 2015, inayolenga kuimarisha uwazi na uwajibikaji katika sekta ya uziduaji.

Alisisitiza kuwa ushirikiano huo unapaswa kuendelezwa ili kuongeza uwazi na uwajibikaji katika usimamizi wa rasilimali za madini, mafuta na gesi asilia nchini.

Naye Meneja wa mgodi huo, Bw. Ashraf Suryaningrat, alisema Geita Gold Mining Limited itaendelea kushirikiana kikamilifu na TEITI katika kufanikisha lengo la uwazi na uwajibikaji katika sekta ya uziduaji, akibainisha kuwa mgodi huo ni miongoni mwa wadau wakubwa wa TEITI nchini.

 

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo, Mhe. Deodatus Mwanyika (Mb), ameeleza kuridhishwa kwake na hatua ya ujenzi wa jengo la kisasa la Vipimo na Viwango katika Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE) jijini Dar es Salaam.

Akizungumza Machi 12, 2026, Mhe. Mwanyika amebainisha kuwa mradi huo wa ghorofa 10 umefikia asilimia 93 ya utekelezaji wake, jambo linaloashiria usimamizi madhubuti na weledi katika ukamilishaji wa Jengo Jengo hilo ili kukidhi ongezeko la wanafunzi wanaodahiliwa kila mwaka.

Vilevile, Mwenyekiti huyo ametoa rai kwa uongozi wa chuo kuendelea kutoa na kuimarisha elimu ya kati (middle-level education) katika fani za biashara hususani ujasiliamali kwa kuwa ni nyenzo adhimu kwa wahitimu wanaojiandaa kuingia kwenye soko la ajira binafsi na

Kutasaidia kuongeza hadhi ya chuo na kuchochea ari ya wanafunzi wengi zaidi kujiunga na taasisi hiyo.

Amesema kuwa uimara wa chuo unategemea ubora wa mafunzo unayoyatoa na uwezo wake wa kuzalisha wataalamu wenye ushindani katika soko la ndani na nje ya nchi.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Dennis Londo (Mb), amefafanua kuwa mradi huo unatekelezwa kupitia bajeti ya Serikali ya mwaka wa fedha 2025/26 na unatarajiwa kuwa na uwezo wa kubeba zaidi ya wanafunzi 4,000 kwa wakati mmoja.

Aidha amebainisha kuwa Jengo hilo la Vipimo na Viwango litakuwa kitovu cha mafunzo ya masoko na nyanja mbalimbali za kibiashara ambazo zinahitajika kwa kiasi kikubwa kulingana na mwelekeo wa sasa wa uchumi wa viwanda.

Naye Mkuu wa Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE), Prof. Edda Lwoga, ameeleza kuwa mradi huo ulioanza Mei 25, 2023, umekuwa mhimili wa mabadiliko makubwa ya kitaaluma chuoni hapo. Alibainisha kuwa kukamilika kwa jengo hilo kutaongeza fursa za udahili kwa wanafunzi wengi wanaohitaji masomo ya biashara na ujasiriamali, ikiwemo kozi fupi ambazo zimekuwa na mahitaji makubwa kwa wadau wa sekta binafsi.

Benki Kuu ya Tanzania (BoT), ikiongozwa na Naibu Gavana wa Sera za Uchumi na Fedha, Dkt. Yamungu Kayandabila, imefanya kikao na wadau mbalimbali kujadiliana kuhusu mpango wa kuanzishwa kwa kampuni ya utoaji na usimamizi wa dhamana za mikopo itakayojulikana kama Tanzania Credit Guarantee PLC.

Kikao hicho kilichofanyika leo, tarehe 12 Machi 2026, katika ofisi za Benki Kuu jijini Dar es Salaam, kimewakutanisha wadau kutoka taasisi mbalimbali ikiwemo Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA), Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA), Kampuni za Bima, Mifuko ya Pamoja ya Uwekezaji wa Mitaji, Mifuko ya Pensheni pamoja na Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF).

Mpango wa kuanzishwa kwa kampuni hiyo unalenga kuendana na ukubwa na kasi ya utekelezaji unaohitajika kufanikisha Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, ambayo inalenga kuimarisha uchumi wa Tanzania na kuongeza mchango wa sekta binafsi katika maendeleo ya taifa.

Vilevile, kampuni hiyo itasaidia kutenganisha majukumu ya Benki Kuu ya udhibiti na utoaji wa dhamana za mikopo, hivyo kuondoa mgongano wa maslahi na kuboresha ufanisi wa kiutendaji. Pia itahamasisha ubunifu pamoja na kuongeza uwezo wa taasisi husika kujibu kwa haraka mahitaji ya soko.

Kwa sasa, Benki Kuu ya Tanzania inasimamia mifuko miwili ya udhamini wa mikopo ambayo ni Mfuko wa Udhamini wa Mikopo kwa Mauzo ya Nje (Export Credit Guarantee Scheme – ECGS) na Mfuko wa Udhamini wa Mikopo kwa Wajasiriamali Wadogo na wa Kati (SME Credit Guarantee Scheme – SME-CGS).

Serikali ilianzisha mifuko hiyo kwa lengo la kudhamini benki na taasisi za fedha ili kuimarisha utoaji wa mikopo kwa wakopaji wenye miradi yenye tija lakini wanaokabiliwa na upungufu wa dhamana. Lengo kuu ni kuwezesha mazingira rafiki ya kukuza na kuendeleza miradi ya maendeleo, kuongeza ajira, kuimarisha upatikanaji wa fedha za kigeni kupitia mauzo ya nje na kuchangia ukuaji wa pato la Taifa.
Naibu Gavana, Dkt. Yamungu Kayandabila, akielezea jambo katika kikao na wadau kilichofanyika Benki Kuu jijini Dar es Salaam tarehe 12 Machi 2026.
Wadau mbalimbali katika kikao na Benki Kuu kilichofanyika jijini Dar es Salaam tarehe 12 Machi 2026.
Mkurugenzi wa Ustawi na Huduma Jumuishi za Fedha BoT, Bw. Kennedy Komba, akifafanua jambo katika kikao na wadau kilichofanyika Benki Kuu jijini Dar es Salaam tarehe 12 Machi 2026.
Meneja wa Idara ya Huduma za Wakala wa Serikali BoT, Bw. Sadick Nyanzowa, akizungumza katika kikao na wadau kilichofanyika Benki Kuu jijini Dar es Salaam tarehe 12 Machi 2026.
Kamishna wa Bima Tanzania, Dkt. Baghayo Abdallah Saqware, akichangia mada katika kikao na wadau kilichofanyika Benki Kuu jijini Dar es Salaam tarehe 12 Machi 2026.
Afisa Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA), CPA Nicodemus Mkama, akichangia mada katika kikao na wadau kilichofanyika Benki Kuu jijini Dar es Salaam tarehe 12 Machi 2026.
Naibu Gavana, Dkt. Yamungu Kayandabila pamoja na wadau baada ya kikao kilichofanyika Benki Kuu jijini Dar es Salaam tarehe 12 Machi 2026.

 Airtel Tanzania, kampuni inayoongoza huduma za mawasiliano nchini, imezindua maduka mapya 17 ya Airtel Smart Shops jijini Dar es Salaam. Maduka haya ni sehemu ya mtandao wa maduka 31 nchini kote, ukiwa na lengo la kupanua huduma za kidijitali na kuongeza ujumuishaji wa kifedha kwa wananchi.


Uzinduzi huo uliofanyika Machi 12, 2026, ulihudhuriwa na Mhe. Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki, Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, pamoja na viongozi wa serikali, wajasiriamali, na vyombo vya habari.

Waziri Kairuki alieleza kuwa uwekezaji huu ni ishara ya nia ya dhati kwa Airtel kuleta mapinduzi makubwa katika sekta ya mawasiliano na kuonyesha imani yake katika mazingira ya biashara Tanzania chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan.

“Maduka haya mapya yanaonyesha dhati ya Airtel katika kuleta huduma karibu na wananchi huku yakiboresha uzoefu wa wateja. Pia unaashiria imani thabiti katika mazingira ya biashara Tanzania,” alisema Waziri Kairuki.


Kwa upande wake, Charles Kamoto, Mkurugenzi Mtendaji wa Airtel Tanzania, alisema maduka haya hayako tu kama maduka ya rejareja. Yameundwa kama vituo vya kisasa vya huduma za kidijitali, vinavyotoa usajili wa SIM, intaneti ya kasi, huduma za kifedha kupitia Airtel Money, mauzo ya simu, na suluhisho za kibiashara kwa SMEs.


Maduka haya yamewekwa katika maeneo yenye shughuli nyingi jijini Dar es Salaam, ili kurahisisha upatikanaji wa huduma kwa wakazi na wajasiriamali. Uzinduzi huu ni sehemu ya mpango wa kitaifa wa “Airtel Kila Kona”, unaolenga kufanikisha upatikanaji wa huduma za mawasiliano hata katika maeneo ya vijijini.

Kampuni pia imewekeza katika kupanua mtandao wake wa 4G, kuanzisha teknolojia ya 5G, na kuongeza uunganishaji wa kimataifa kupitia mfumo wa nyaya za chini ya bahari wa 2Africa Submarine Cable System.



Adriana Lyamba, Mkurugenzi wa Uzoefu wa Wateja Airtel Tanzania, alisema maduka haya yameundwa kutoa huduma haraka, bila karatasi, na kwa ufanisi. Maduka haya yanatarajiwa pia kuunda ajira na kusaidia SMEs na wajasiriamali wa ndani kwa kuwapatia zana za kifedha za kidijitali na huduma za mawasiliano za kisasa.

Na Maandishi Wetu 

MKURUGENZI  Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi, Hassan Saidy amesema Wananchi hususan wanaoishi vijijini wana matumaini na Serikali kupitia REA katika kuwaboreshea hali ya maisha na amewataka Watumishi wa Wakala kuhakikisha wanafanya kazi kwa bidii, uadilifu na maarifa ili kutimiza malengo ya Serikali kuhudumia wananchi wake.

Ametoa rai hiyo Machi 12, 2026 mkoani Morogoro wakati wa kufungua Kikao cha Tatu cha Baraza la Pili la Wafanyakazi wa REA lenye ajenda kuu ya kupitia na kujadili mapato na matumizi kwa Mwaka 2026/2027.

"Watumishi wenzangu mnafanya kazi nzuri, tuendelee kuhakikisha tunawatumikia wananchi, matumaini yao kwetu ni makubwa na leo hii tupo hapa kujadili Mapato na Matumizi katika kutekeleza na kukamilisha miradi na kwa bajeti ya REA imezingatia vipaumbele vya Serikali ikiwemo kuharakisha kupeleka umeme vitongojini, kuongeza idadi ya wateja na kutanua wigo upatikanaji wa Nishati Safi ya Kupikia,” amesema Mhandisi Saidy.

Amesema makadirio ya Mapato na Matumizi ya Bajeti kwa Mwaka 2026/2027 yanayojadiliwa katika Baraza hilo yamelenga kuboresha mazingira ya kazi na uwezo wa Taasisi katika kutekeleza majukumu yake sambamba na maslahi ya Watumishi.

Akizungumzia mafanikio yaliyofikiwa ndani ya kipindi cha miezi 12 (kutoka kikao cha Baraza kilichopita cha Mwezi Machi, 2025 hadi kikao cha sasa Machi, 2026), Mha. Saidy amesema REA imefanikiwa kusambaza umeme kwenye vitongoji 3,532 ambayo ni sawa na wastani wa vitongoji 10 kwa siku.

"Ndani ya kipindi cha miezi 12 tumefanikiwa kusambaza mitungi 400,000, majiko banifu 300,000, kujenga mifumo ya kisasa ya kupikia kwa Taasisi 452 zinazohudumia zaidi ya Watu 100, tumeanza kutekeleza Mradi wa kupeleka Umeme - Jua kwa kaya takriban 20,000 katika visiwa 143 na ndani ya kipindi hiki miradi takriban mitatu ya kusambaza ùmeme imekamilika,” amesema Mkurugenzi Mkuu wa REA.

Akizungumza katika kikao hicho, Katibu Mkuu wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya Tanzania (TUGHE), Hery Mkunda ameipongeza REA kwa kuendelea kutekeleza majukumu yake kwa weledi na uzalendo.

“REA mnafanya kazi kubwa sana, mmefanikisha azma ya Serikali ya kubadilisha na kuboresha maisha ya wananchi wa maeneo ya vijijini, kwa hili kila mwananchi anaetoka kijijini ni shahidi,” amepongeza Mkunda.

Kikao cha Tatu cha Baraza la Pili la Wafanyakazi wa REA kilihudhuriwa na Mwakilishi wa Katibu Mkuu Wizara ya Nishati, Wilson Nyamanga, Mwakilishi wa Msajili wa HAZINA, Gerald Nzalalila pamoja na Katibu Mkuu wa TUGHE mkoa wa Dodoma, Samwel Nyangwa ambao walipata fursa ya kuzungumza na Watumishi.









Top News