Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule, amesema Tanzania ni miongoni mwa nchi chache barani Afrika zilizofanikiwa kusambaza huduma ya umeme  vijijini, hatua ambayo imewezesha wananchi wengi kupata huduma hiyo kutoka ngazi za mikoa, wilaya, kata na vijiji, huku sasa juhudi zikielekezwa katika kufikisha umeme kwenye vitongoji.

Akizungumza na wananchi wa Kata ya Hogoro wilayani Kongwa mkoani Dodoma wakati wa ziara ya kusikiliza na kutatua kero za wananchi, Senyamule alisema serikali inatarajia kupeleka umeme katika vitongoji sita vya kata hiyo katika mwaka ujao wa fedha.

Alieleza kuwa matarajio ya serikali ni kuhakikisha vitongoji vyote vinapata huduma ya umeme ifikapo mwaka 2030, jambo litakalosaidia kuongeza maendeleo ya kiuchumi na kijamii kwa wananchi.

“Zamani wananchi walitegemea chemli na vibatari kwa ajili ya mwanga, lakini sasa serikali imeona umuhimu wa kupeleka umeme karibu na wananchi ili waweze kupata mwanga wa uhakika na kufanya shughuli mbalimbali za kiuchumi zinazowaongezea kipato na kuchangia ukuaji wa uchumi wa taifa.”

Katika sekta ya elimu, Mkuu huyo wa Mkoa alisema Serikali ya Awamu ya Sita imefanikisha ujenzi wa shule nyingi zaidi kuliko vipindi vilivyotangulia, huku akiwataka wazazi na walezi kuhakikisha watoto wote wanapata fursa ya elimu.

Alisisitiza kuwa dhamira ya serikali ni kuona kila Mtanzania anajua kusoma na kuandika katika miaka ijayo ili kuwaandaa wananchi kukabiliana na ushindani wa dunia ya sasa inayokua kwa kasi katika nyanja za sayansi na teknolojia.

“Dunia ya leo imekuwa kama kijiji kutokana na maendeleo ya teknolojia. Elimu na ujuzi ni nyenzo muhimu zinazoweza kumpa mtu fursa ya kufanya kazi na kuishi popote duniani”.

Aidha, Senyamule alisema serikali imeendelea kuboresha huduma za afya kwa kujenga na kuimarisha zahanati, vituo vya afya na hospitali pamoja na kuweka mazingira rafiki ya utoaji huduma.

Kutokana na maboresho hayo, alisema hakuna sababu ya wanawake wajawazito kujifungulia nyumbani kwani huduma bora za afya sasa zinapatikana karibu na wananchi, hatua inayolenga kupunguza vifo vya mama na mtoto wakati wa kujifungua.





-Nchi nane wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki zitakutana Bujumbura, Burundi katika kuadhimisha siku ya Kiswahili Duniani pamoja na Kongamano la Kakama.


Na Vero Ignatus

Kamisheni ya Kiswahili ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (Kakama) imetangaza maadhmisho ya Siku Kiswahili kuwakutanisha wananchi kutoka mataifa nane ya Afrika Mashariki mjini Bujumbura, Burundi.

Akizungumza na waandishi wa habari kutoka vyombo mbalimbali, Katibu Mtendaji wa Kamisheni ya Kiswahili (Kakama), Dk Caroline Asiimwe amesema maadhimisho hayo yatafanyika kuanzia Julai 5-7 Julai, 2026.

Amesema maadhmisho ya Kiswahili yatatanguliwa na Kongamano la Tatu ka Kakama na kufuatiwa na Siku ya Kiswahiki Duniani Julai 7.

Amesema maadhimisho ya kongamano la Kakama yamkuwa yakifanyika kila baada ya miaka miwili na kutoa fursa kwa kila nchi wanachama.

Amesisitiza kwamba kupitia maadhimisho hayo yamewezesha wananchi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki kunufaika na fursa mbalimbali kupitia Kiswahili.

Dk Asiimwe: Kiswahili chafikia hadhi kimataifa kuchangia maendeleo

Aidha lugha ya Kiswahili imetajwa kufikia hadhi ya kimataifa kiwango cha kuwezesha kuwa na mchango wa maendeleo katika nchi wanachama Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Amesema lugha ya Kiswahili inaweza kumwezesha mwekezaji kuchangamkia fursa mbalimbali zilizopo katika nchi husika kutokana na kutumika na takribani nchi nane wanachama wa jumuiya.

Dk Asiimwe amesema lugha ya Kiswahili inamwezesha hata mjasiriamali na mfanyabiashara aliyepo kijijini kuamua kuchagua lugha atakayo kupitia akili unde ili kumwezesha kuwasiliana kikamilifu.

Amesema kutokana na maendeleo ya teknolojia, yamewasukuma katika maadhimisho ya Kiswahili Duniani na Kongamano la Tatu yatakayoanyika Bujumbura Julai 5-7 mwaka huu kubeba mjadala wa akili unde na wingi lugha.


📍 Chinangali Park, Dodoma

TAWIRI  imeendelea kutoa elimu  kwa wadau wakiwepo  wananchi ambapo wakulima wamepata elimu ya umuhimu wa wadudu katika  uhifadhi endelevu wa wanyamapori sambamba na mchango wa wadudu katika kilimo ikiwa ni pamoja na uchavushaji.

Vilevile wananchi wamepata uelewa  juu ya juhudi zinazofanywa na TAWIRI chini ya Wizara ya Maliasili na Utalii za kuwahifadhi wanyamapori kwa kutumia taarifa sahihi za kisayansi.

“tunashukuru kwa elimu nzuri, kabla ya elimu hii nilijua wanyamapori wanakaa porini wanajihudumia lakini leo nimepata uelewa  wanyamapori wanatibiwa, wanahesabiwa, wanafuatiliwa mienendo yao kwa kutumia teknolojia” 

amesema  Enderesa Salla miongoni mwa wananchi waliotembelea banda la TAWIRI

TAWIRI tunawakaribisha wananchi na wadau mbalimbali kuja kupata elimu ya sayansi ya wanyamapori  kwa ustawi wa uhifadhi na kukuza Utalii.



Na Said Mwishehe,Michuzi TV


RAIS wa Jamhuri ya Namibia, Dkt. Netumbo Nandi-Ndaitwah amewasili nchini Tanzania kwa ziara ya Kitaifa ya siku tatu kwa mwaliko wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Akiwa nchini Rais Dkt. Nandi-Ndaitwah anatarajiwa kufanya mazungumzo ya uwili na mwenyeji wake, Rais Dkt. Samia kwa lengo la kuimarisha zaidi ushirikiano katika sekta mbalimbali zenye manufaa kwa Wananchi wa Tanzania na Namibia.

Pia Rais Ndaitwah na mwenyeji wake Rais Dk.Samia wanatarajiwa kushuhudia utiaji saini wa hati mbalimbali za makubaliano ya ushirikiano kati ya Nchi hizo mbili.

Aidha pamoja na mambo mengine inaelezwa kwamba ziara hiyo inakwenda kufungua fursa zaidi za kiuchumi kati ya nchi hizo ambazo zimekuwa na urafiki wa kindugu na wa kihistoria kwa muda mrefu.

Akizungumzia ziara hiyo alipokuwa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam wakati wa mapokezi ya Rais Ndaitwah, Balozi wa Tanzania nchini Namibia, Caesar Waitara, amesema ziara hiyo ni ishara ya uhusiano wa muda mrefu na wa kihistoria uliopo kati ya mataifa hayo mawili, huku akisisitiza kuwa ziara hiyo inaleta manufaa makubwa katika utekelezaji wa diplomasia ya uchumi.

Balozi Waitara anasema Rais wa Namibia anaitazama Tanzania kama nyumbani kwake kutokana na historia yake ya kuishi nchini kwa miaka sita alipokuwa mwakilishi wa chama cha SWAPO katika nchi za Afrika Mashariki.

Anabainisha kuwa makao yake yalikuwa katika eneo la Magomeni jijini Dar es Salaam, jambo linaloimarisha zaidi uhusiano wake binafsi na Tanzania.

“Ujio wake unaonyesha jinsi uhusiano kati ya Tanzania na Namibia ulivyo imara na wa muda mrefu. Kila mara anapokuja Tanzania anajisikia kama yuko nyumbani,” anasema Waitara.

Anaeleza kuwa Namibia inaendelea kuthamini mchango wa Tanzania katika harakati za ukombozi wa taifa hilo, hususan kupitia kambi za wapigania uhuru zilizokuwa Kongwa pamoja na msaada wa mafunzo ya kijeshi uliotolewa kwa wapigania uhuru wa Namibia.

Kwa mujibu wa balozi huyo, pamoja na historia ya ukombozi, mataifa hayo sasa yamejikita zaidi katika kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi kupitia biashara, uwekezaji na kubadilishana uzoefu katika sekta mbalimbali za maendeleo.

Waitara anasema Tanzania inaendelea kusukuma mbele ajenda ya diplomasia ya uchumi kupitia balozi zake nje ya nchi kwa lengo la kuvutia uwekezaji na kufungua fursa za biashara.

Anataja uwekezaji wa Watanzania nchini Namibia kuwa ni mfano wa mafanikio ya ushirikiano huo, ambapo baadhi ya Watanzania wameanzisha biashara na taasisi za elimu.

Anabainisha kuwa kuna chuo kikuu nchini Namibia kinachomilikiwa kwa asilimia 100 na Mtanzania, ambacho kinatoa elimu ya shahada, shahada za uzamili na uzamivu, huku kikiwa na zaidi ya wanafunzi 10,000.

Aidha, Watanzania wengine wanaendelea kufanya biashara mbalimbali nchini humo, wakati WanaNamibia wamewekeza Tanzania katika sekta za utalii na mawasiliano.

Katika kuimarisha mahusiano ya kitamaduni, Waitara anasema ubalozi wa Tanzania kwa kushirikiana na Baraza la Kiswahili la Taifa (BAKITA) umeanza kutoa mafunzo ya lugha ya Kiswahili kwa njia ya mtandao nchini Namibia.

Anafafanua wanafunzi 26 walihitimu mafunzo ya awali mwaka jana, huku kundi jipya la wanafunzi 40 likitarajiwa kuanza masomo hivi karibuni.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, akizungumzia ziara ya Rais wa Namibia anasisitiza ni uthibitisho kuwa mahusiano ya kihistoria kati ya mataifa hayo sasa yamepanuka na kuwa ushirikiano mkubwa wa kiuchumi.

Anasema maboresho makubwa yaliyofanyika katika Bandari ya Dar es Salaam yanaifanya Tanzania kuwa lango muhimu la biashara kwa nchi nyingi za ukanda wa Kusini mwa Afrika, jambo linaloweza kuongeza ushirikiano wa kibiashara kati ya Tanzania na Namibia.

Wakati Kamanda wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Jumanne Muliro, anasema mafanikio ya diplomasia ya uchumi hayawezi kupatikana bila kuwepo kwa usalama.

Ananasisitiza kuwa amani na utulivu wa Tanzania ndiyo msingi unaowezesha viongozi wa kimataifa kutembelea nchi na wawekezaji kuendelea kuwekeza.

“Usalama ni mtaji muhimu wa uchumi. Bila usalama hakuna biashara, hakuna uwekezaji wala maendeleo. Ni jukumu la kila mwananchi kuendelea kuilinda amani ya nchi yetu,” anasema Kamanda Muliro.

Ziara ya Rais wa Namibia nchini Tanzania inatarajiwa kuimarisha zaidi ushirikiano wa kihistoria, kiuchumi na kitamaduni kati ya mataifa hayo mawili, huku ikifungua fursa mpya za biashara, uwekezaji na maendeleo kwa wananchi wa pande zote mbili.


Na Chalila Kibuda ,Michuzi TV

SERIKALI imeitaka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kujiandaa mapema kukabiliana na mabadiliko makubwa ya kiuchumi na kiteknolojia yanayotarajiwa katika miaka 30 ijayo, ikieleza kuwa zaidi ya asilimia 70 ya shughuli za kiuchumi zitakuwa zikifanyika kwa njia za kidijitali.

Hayo ameyasema na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Nsubili Joshua, kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omary, wakati wa Kongamano la Miaka 30 ya TRA tangu kuanzishwa kwake mwaka 1996, lililoandaliwa na TRA kupitia Chuo cha Kodi.

Joshua alisema mabadiliko ya teknolojia yanayoendelea duniani yanahitaji TRA kuwa mbele ya wakati kwa kuandaa mifumo madhubuti ya usimamizi wa kodi itakayoweza kukusanya mapato kutoka biashara za mtandaoni na huduma zinazovuka mipaka ya nchi.

Alisema pamoja na mafanikio makubwa yaliyopatikana katika kipindi cha miaka 30 ya TRA, bado kuna haja ya kuimarisha mifumo ya kodi ili iendane na kasi ya maendeleo ya uchumi wa kidijitali unaotarajiwa kutawala katika miaka ijayo.

“Katika miaka 30 ijayo zaidi ya asilimia 70 ya shughuli za kiuchumi zitafanyika kwa njia za kidijitali hivyo TRA inapaswa kuwa tayari kuhakikisha mapato ya Serikali yanakusanywa kwa ufanisi bila kuathiri mazingira ya biashara na ubunifu,” amesema Joshua.

Alifafanua kuwa lengo la Serikali si kuzuia maendeleo ya teknolojia, bali kuhakikisha kunakuwa na usawa wa kodi na ulinzi wa mapato ya taifa huku mazingira bora ya uwekezaji na ushindani wa haki yakiendelea kudumishwa.

Aidha, aliitaka TRA kuongeza uwekezaji katika matumizi ya akili mnemba (AI), uchambuzi wa takwimu na mifumo ya ufuatiliaji wa miamala kwa wakati halisi ili kubaini mianya ya ukwepaji kodi na kuimarisha uwazi katika ukusanyaji wa mapato.

Joshua alisema matumizi ya teknolojia hizo yatasaidia kugundua udanganyifu mapema, kupunguza mawasiliano yasiyo ya lazima kati ya walipakodi na maafisa wa kodi pamoja na kuongeza ufanisi wa utoaji huduma.

Pia aliitaka TRA kuendelea kubuni mifumo rahisi ya usajili, ukadiriaji na ulipaji kodi kwa sekta isiyo rasmi ikiwemo wafanyabiashara wadogo na wakulima, ili kupanua wigo wa walipakodi na kuongeza mapato ya ndani.

Alisema mafanikio ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 yatategemea kwa kiasi kikubwa uwezo wa nchi kukusanya mapato ya ndani na kuyasimamia kwa ufanisi, jambo linaloifanya TRA kuwa na jukumu muhimu katika safari ya maendeleo ya taifa.

Joshua alisisitiza kuwa ushirikiano kati ya TRA, wafanyabiashara, watafiti na wadau wengine wa kodi ni muhimu katika kujenga mfumo wa kodi unaoendana na mahitaji ya uchumi wa kisasa na kuhakikisha Tanzania inanufaika kikamilifu na mapinduzi ya teknolojia yanayoendelea duniani.
Kamishina Mkuu wa TRA CPA Yusuph Mwenda akitoa maelezo kuhusiana tangu kuanzishwa mamlaka ya Mapato katika kongamano la miaka 30 tangu Kuanzishwa lililofanyika Ukumbi wa Serena ,jijini Dar es Salaam.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha Nsubili Jushua akizungumza kwa niaba ya Waziri wa Fedha Balozi Khamis Mussa Omary wakati akizindua Kongamano la Miaka 30 ya Mamlaka ya Mapato (TRA) lililofanyika Ukumbi wa Serena Jijini Dar es Salaam.

Mkuu wa Chuo cha Kodi Profesa Isaya Jairo akizungumza kuhusiana na kuratibu Kongamano hilo kwa lengo kukutanisha wadau kujadiliana miaka 30 ijayo juu utendaji wa TRA.jijini Dar es Salaam.



Picha za pamoja za Makundi katika kongamano la TRA


- Mikopo ya mifugo NMB yavuka Sh180 bilioni.

Ubena Zomozi; Benki ya NMB imetoa zaidi ya Sh180 bilioni kufadhili wafugaji na biashara katika mnyororo wa thamani wa mifugo, ikiwemo unenepeshaji, uzalishaji wa malisho, ununuzi wa mbegu bora na ujenzi wa miundombinu ya kisasa.

Afisa Mkuu wa Wateja Binafsi na Biashara wa NMB, Filbert Mponzi, alisema hayo katika ufunguzi wa Tri-Nations Livestock Expo 2026 uliofanywa na Waziri Mkuu, Dk. Mwigulu Nchemba, katika viwanja vya Mbogo Ranches, Ubena Zomozi, Chalinze. NMB ni mdhamini mkuu kwa mwaka wa nne mfululizo.

Mponzi alisema mikopo hiyo inatolewa kwa riba nafuu ya asilimia tisa, huku mkakati wa NMB wa agribusiness na agri-wholesale ukilenga kufadhili wafugaji, wazalishaji wa malisho, wanunuzi, wasindikaji na biashara kubwa katika sekta hiyo.

Dk. Nchemba aliwataka wafugaji kutumia elimu na teknolojia inayopatikana katika maonesho hayo kukabiliana na uhaba wa malisho na kuongeza tija.

NMB imesema itaendelea kutoa elimu ya fedha, ushauri wa biashara, mikopo na bima kupitia matawi 248, mawakala zaidi ya 75,000 na huduma za kidijitali ili kusogeza huduma karibu zaidi na wafugaji nchini.

Waziri Mkuu, Dk. Mwigulu Nchemba, akisikiliza maelezo kutoka kwa Afisa Mkuu wa Wateja Binafsi na Biashara wa NMB, Filbert Mponzi, kuhusu mikopo, elimu ya fedha na huduma za kibenki kwa wafugaji alipotembelea banda la NMB katika Tri-Nations Livestock Expo 2026, Mbogo Ranches, Ubena Zomozi wilayani Chalinze, mkoani Pwani. 







 Benki ya Taifa ya Biashara (NBC), mdhamini mkuu wa Ligi ya NBC Championship, imejivunia mafanikio yanayoendelea kushuhudiwa katika mchezo wa soka nchini huku ikikabidhi kombe la ubingwa wa msimu wa 2025/2026 kwa Geita Gold FC, timu iliyotwaa taji hilo baada ya kumaliza ligi ikiwa kileleni kwa alama 77.

Ubingwa huo unaipa Geita Gold FC tiketi ya kushiriki Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2026/2027 sambamba na Kagera Sugar FC iliyomaliza nafasi ya pili kwa alama 71 na hivyo nayo kufuzu kushiriki ligi hiyo.

Kombe hilo lilikabidhiwa jana katika Uwanja wa Nyankumbu, Geita, baada ya Geita Gold FC kuhitimisha msimu kwa ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Big Man FC ya Lindi katika mechi iliyoshuhudiwa na mamia ya mashabiki pamoja na viongozi mbalimbali wa soka, serikali na vyama vya siasa.

Katika hafla hiyo, Mkuu wa Biashara wa NBC Kanda ya Ziwa, Mafwimbo Bihemo, aliyemwakilisha Mkurugenzi Mtendaji wa NBC, Theobald Sabi, alisema benki hiyo inafurahishwa na namna uwekezaji wake katika soka unavyoendelea kuzaa matokeo chanya kupitia ongezeko la ushindani, kuibuka kwa vipaji vipya na kuimarika kwa viwango vya ligi za ndani.

Alisema NBC, ambayo imewekeza zaidi ya Shilingi bilioni 32 katika udhamini wa Ligi Kuu ya NBC, NBC Championship na Ligi ya Vijana, itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kuhakikisha soka linaendelea kukua na kutoa mchango mkubwa kwa maendeleo ya kijamii na kiuchumi nchini.

“Tunawapongeza washiriki wote wa NBC Championship kwa ushindani mkubwa waliouonyesha msimu mzima. Kipekee tunawapongeza Geita Gold FC kwa kutwaa ubingwa na Kagera Sugar FC kwa kufuzu Ligi Kuu ya NBC. Mafanikio haya yanaonyesha kiwango kikubwa cha ushindani kinachoendelea kujengeka katika soka la Tanzania,” alisema Bihemo.

Alisema NBC inaona matokeo ya uwekezaji huo kupitia maendeleo yanayoonekana katika ligi za ndani, kuimarika kwa ushindani wa vilabu na mafanikio yanayozidi kupatikana kwa timu za taifa katika mashindano ya kimataifa.

“Tunajivunia kuona soka la Tanzania likiendelea kupiga hatua. Ushindani unaoanzia ligi za vijana, NBC Championship hadi Ligi Kuu ya NBC umeendelea kuongeza ubora wa mchezo na kuzalisha wachezaji wenye uwezo wa kushindana katika viwango vya juu zaidi. Haya ndiyo matokeo tunayolenga kuyaona kupitia uwekezaji wetu,” aliongeza.

Bihemo alisema NBC itaendelea kuboresha mchango wake kwa wadau wa soka kupitia huduma mbalimbali za kifedha zikiwemo mikopo kwa vilabu, bima za afya kwa wachezaji na benchi la ufundi pamoja na elimu ya fedha inayolenga kuimarisha ustawi wa wadau wa mchezo huo.

Kwa upande wake, Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Wallace Karia, aliipongeza NBC kwa mchango wake mkubwa katika kukuza soka la Tanzania kupitia udhamini wa ligi hizo tatu, akibainisha kuwa ushindani wa sasa katika ligi za ndani ni miongoni mwa matokeo makubwa ya uwekezaji huo.

“Leo tunaona NBC Championship ikiwa na ushindani mkubwa kuanzia mwanzo hadi mwisho wa msimu. Vilabu vinaendesha shughuli zake kwa weledi zaidi, vina uwezo wa kusajili wachezaji bora na kujiandaa vizuri kwa mashindano. Haya ni maendeleo makubwa kwa soka letu,” alisema Karia.

Aliwataka Geita Gold FC na Kagera Sugar FC kutumia fursa ya kupanda Ligi Kuu ya NBC kujiimarisha zaidi ili kuongeza ushindani katika ligi hiyo pamoja na kuwekeza katika miundombinu ya viwanja ili mashabiki wao waweze kufurahia mechi za nyumbani katika mazingira bora.

Akizungumza kwa niaba ya wachezaji wa Geita Gold FC, nahodha wa timu hiyo Yusuph Mhilu aliwashukuru mashabiki, viongozi, benchi la ufundi na wadhamini kwa mchango wao katika kufanikisha ubingwa huo.

Alisema timu hiyo inatambua ushindani mkubwa uliopo katika Ligi Kuu ya NBC na tayari imeanza maandalizi ya kuhakikisha inakwenda kutoa ushindani wa kiwango cha juu msimu ujao.


Mkuu wa Biashara wa NBC Kanda ya Ziwa, Mafwimbo Bihemo (mwenye fulana nyeusi) pamoja na Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Wallace Karia (alievaa kofia) wakiwapongeza wachezaji wa timu ya Geita Gold FC ya mkoani Geita baada ya timu hiyo kukabidhiwa rasmi kombe la Ligi Daraja la Kwanza (NBC Championship)msimu wa 2025/2026. Hafla ya kukabidhi kombe hilo ilifanyika jana katika Uwanja wa Nyankumbu, Geita, baada ya Geita Gold FC kuhitimisha msimu kwa ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Big Man FC ya Lindi katika mechi iliyoshuhudiwa na mamia ya mashabiki pamoja na viongozi mbalimbali wa soka, serikali na vyama vya siasa




Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Wallace Karia (katikati alievaa kofia) akiongoza zoezi la uvalishaji wa medali kwa wachezaji wa timu ya Geita Gold FC ya mkoani Geita baada ya timu hiyo kukabidhiwa rasmi kombe la Ligi Daraja la Kwanza (NBC Championship)msimu wa 2025/2026. Hafla ya kukabidhi kombe hilo ilifanyika jana katika Uwanja wa Nyankumbu, Geita, baada ya Geita Gold FC kuhitimisha msimu kwa ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Big Man FC ya Lindi katika mechi iliyoshuhudiwa na mamia ya mashabiki pamoja na viongozi mbalimbali wa soka, serikali na vyama vya siasa



Baadhi ya mashabiki wa Geita Gold FC wakifurafia ubingwa huo.






Haikuwa kazi rahisi! Wachezaji wa Geita Gold FC wakiwa kwenye nyakati tofauti uwanjani.




Vikosi vya Geita Gold FC (juu) na Big Man FC (chini) vilivyokutana kwenye mchezo huo




Muonekano wa kombe la Ligi Daraja la Kwanza (NBC Championship) msimu wa 2025/2026

 


Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) imeungana na Taasisi mbalimbali za umma kushiriki katika Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayofanyika katika viwanja vya Chinangali Park, jijini Dodoma kuanzia, Juni 16, 2026.

Katika maonesho hayo, TCAA inatoa elimu kwa wananchi kuhusu majukumu yake ya msingi, yakiwemo udhibiti wa shughuli zote za usafiri wa anga nchini. Hii inajumuisha pia usimamizi wa matumizi ya droni, ambalo ni eneo linalokua kwa kasi na kuhitaji ufuatiliaji wa karibu siyo tu kwa ajili ya usalama wa anga, bali pia kulinda faragha ya watu na kuepusha matumizi ya vifaa hivyo katika maeneo yasiyoruhusiwa kisheria, kama vile maeneo ya kijeshi, taasisi za serikali, na miundombinu nyeti.

Huduma nyingine zinazotolewa na TCAA ni pamoja na utoaji wa huduma za uongozaji ndege kwa ajili ya kuhakikisha usalama wa safari za anga ndani ya eneo la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Aidha, Mamlaka hiyo inatumia fursa hiyo kuwahamasisha vijana na wadau wa sekta ya usafiri wa anga kuchangamkia fursa za mafunzo zinazotolewa na Chuo cha Usafiri wa Anga Tanzania (CATC), kinachomilikiwa na TCAA. Mafunzo hayo yanalenga kuongeza idadi ya wataalamu wa ndani katika sekta muhimu ya usafiri wa anga.

Maadhimisho ya mwaka huu yanaongozwa na kaulimbiu: “Kuchochea uwajibikaji Jumuishi kwa Huduma Endelevu” ikisisitiza umuhimu wa matumizi ya teknolojia katika kuboresha huduma kwa wananchi na kuimarisha uwajibikaji katika utumishi wa umma.

Wiki ya Utumishi wa Umma huadhimishwa kila mwaka ili kutambua mchango wa watumishi wa umma katika maendeleo ya taifa. Maadhimisho ya mwaka huu yanatarajiwa kufikia kilele chake tarehe 23 Juni 2026.
Meneja wa TCAA Kituo cha Dodoma Aswile Kamendu (katikati) akitoa maelezo kwa Mkurugenzi wa Ufuatiliaji na Tathmini kutoka Wizara ya Uchukuzi Devota  Gabriel aliyefika katika banda la Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) kwenye maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayofanyika katika viwanja vya Chinangali Park, jijini Dodoma. 
Mkurugenzi wa Huduma za Usafiri kutoka Wizara ya Uchukuzi Biseko Chiganga  akisaini kitabu katika banda la Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) kwenye maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayofanyika katika viwanja vya Chinangali Park, jijini Dodoma. 
Afisa Rasilimali Watu TCAA Lucy Ngowo (wa pili kulia) akikabidhi zawadi kwa Mkurugenzi wa Huduma za Usafiri Wizara ya Uchukuzi ambaye pia ni Mjumbe wa Bodi Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) Biseko Chiganga
Mkurugenzi wa Huduma za Usafiri kutoka Wizara ya Uchukuzi Biseko Chiganga akiwa kwenye picha pamoja na watumishi wa  Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) alipotembelea banda la Mamlaka hiyo kwenye maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayofanyika katika viwanja vya Chinangali Park, jijini Dodoma. 

Baadhi ya wafanyakazi wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) wakiendelea kutoa elimu katika Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yaliyofanyika kwenye Viwanja vya Chinangali jijini Dodoma.

Ofisi ya Waziri Mkuu pamoja na wadau wa maafa nchini katika Kikao cha Jukwaa la Taifa la Wadau wa Usimamizi wa Maafa kilicholenga kupitia na kuthibitisha Mwongozo wa Urejeshaji Hali Baada ya Maafa, Mwongozo wa Uendeshaji na Uratibu wa Uhawilishaji Fedha kwa Walioathirika wa Maafa, pamoja na Mfumo wa Usimamizi wa Taarifa za Maafa (DMIS) tarehe 19 Juni, 2026 Jijini Dodoma.


DAR ES SALAAM, Juni 18, 2026 – Katibu Msaidizi wa Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Kanda Maalum, Bi. Elizabeth Komba, amewataka viongozi nchini kuwa mfano wa maadili mema kwa maneno, matendo na mwenendo wao wa kila siku ili kuimarisha utawala bora na kujenga imani ya wananchi kwa taasisi za umma.
Bi. Komba alitoa kauli hiyo wakati akifungua mafunzo ya maadili kwa viongozi yaliyofanyika katika Ukumbi wa Tume ya Ushindani jijini Dar es Salaam tarehe 18 Juni 2026.

Alisema Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma, inaendelea kuhamasisha ushiriki wa wananchi na viongozi katika kusimamia na kukuza maadili ili kuimarisha uwajibikaji na utoaji bora wa huduma katika sekta ya umma.

“Viongozi wanapaswa kuwa kioo cha jamii kwa kuzingatia maadili katika maneno na matendo yao. Kwa kufanya hivyo, wataweza kusimamia maadili katika taasisi wanazoziongoza na kuhamasisha watumishi wengine kufuata misingi hiyo,” alisema Bi. Komba.

Aidha, alibainisha kuwa maadili na uadilifu ni nguzo muhimu katika maendeleo ya taifa lolote duniani, kwani humjengea kiongozi heshima, uaminifu na kuthaminiwa na wananchi anaowahudumia.

Alisisitiza kuwa viongozi wanapaswa kutenda haki kwa wote bila ubaguzi, upendeleo au misingi yoyote inayoweza kuathiri utoaji wa huduma kwa wananchi.

Bi. Komba alisema mafunzo hayo yanalenga kuwajengea viongozi uwezo wa kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa, hatua itakayosaidia kuimarisha utoaji wa huduma za umma na kuongeza imani ya wananchi kwa taasisi za Serikali.

Aliongeza kuwa viongozi wenye maadili na uadilifu ni msingi wa maendeleo endelevu, huku akiwataka washiriki wa mafunzo hayo kuyatumia maarifa waliyopata kuboresha utendaji kazi katika maeneo yao ya kazi.

Mafunzo hayo ni sehemu ya jitihada za Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma za kuendelea kuimarisha misingi ya maadili, uwajibikaji na uadilifu miongoni mwa viongozi wa umma nchini.










Top News