Wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Wasichana Mrijo Juu iliyopo wilayani Chemba mkoani Dodoma wamepata nafuu ya changamoto zinazowakabili wakati wa hedhi baada ya kupatiwa msaada wa vifaa maalumu vinavyoweza kutumika kwa muda mrefu, hatua inayolenga kuwawezesha kuendelea na masomo bila kukatishwa tamaa au kukosa vipindi vya darasani.
Msaada huo umetolewa na TotalEnergies Tanzania kwa kushirikiana na mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP), ukiwa sehemu ya juhudi za kuimarisha elimu ya mtoto wa kike na kuhakikisha anabaki shuleni hadi kukamilisha masomo yake.
Kila mwanafunzi alinufaika na kifurushi chenye taulo za kike zinazoweza kufuliwa na kutumika tena kwa muda wa zaidi ya miaka mitatu, pamoja na sabuni, nguo za ndani na ndoo kwa ajili ya kusaidia usafi na uhifadhi wa vifaa hivyo. Vifaa hivyo vinalenga kupunguza changamoto za upatikanaji wa pedi za mara kwa mara pamoja na kusaidia usafi wa mazingira.
Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi wa Sheria na Uhusiano wa TotalEnergies Tanzania, Detrude Mpangile, amesema taulo hizo zimeundwa kwa ubora wa juu na zinaweza kumhudumia mwanafunzi kwa kipindi chote cha elimu ya sekondari kuanzia kidato cha kwanza hadi cha nne. Alibainisha kuwa mpango huo pia unachangia utunzaji wa mazingira kutokana na kupunguza taka zinazotokana na pedi za kutupwa mara moja.
Kwa upande wake, Mtaalamu na Msimamizi wa Miradi ya Uwekezaji na Uwajibikaji kutoka EACOP, Mhandisi Peter Kiungai, amesema mpango huo uliozinduliwa Machi mwaka huu ni sehemu ya mwendelezo wa kurudisha kwa jamii, ukiwa na lengo la kuhakikisha wasichana wanapata mazingira bora ya kusoma bila vikwazo vinavyotokana na changamoto za hedhi.
Akimwakilisha uongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Chemba, Regina Bahaye aliishukuru kampuni ya TotalEnergies Tanzania na EACOP kwa kuendelea kuwafikia wanafunzi na kuwapatia msaada huo, akisisitiza kuwa hatua hiyo itasaidia kupunguza utoro shuleni na kuongeza umakini darasani kwa wanafunzi wa kike.
Kwa niaba ya wanafunzi wenzake, Scolastica amesema msaada huo umewaletea faraja kubwa kwani utawasaidia kuhudhuria masomo kwa utulivu zaidi wakati wa hedhi, huku ukipunguza mzigo wa gharama kwa wazazi na kuchangia utunzaji wa mazingira kutokana na matumizi ya taulo zinazoweza kufuliwa na kutumika tena.
Msaada huo unaendelea kuonekana kuwa sehemu muhimu ya jitihada za kuinua elimu ya mtoto wa kike katika wilaya ya Chemba, ukilenga kuhakikisha hakuna mwanafunzi anayekosa masomo kutokana na changamoto za kibaolojia zinazoweza kudhibitiwa.








.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)






.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)








.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)








