Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na wananchi wa maeneo mbalimbali ya Jiji la Dodoma pembezoni mwa Uwanja wa Ndege wa Dodoma kabla ya kuelekea Jijini Dar es Salaam tarehe 08 Mei, 2026.



MAHAKAMA ya Wilaya ya Ilala imewahukumu raia wa China XU Fuyu (39) na mfanyakazi wake wa mgahawa wa Kibonge, Blandina Mwalutola (24) wamehukumiwa kulipa faini ya Sh milioni  sita kwa kushindwa kutoa risiti ya kielektroniki, baada ya kutoa huduma ya chipsi kuku, sahani ya baga, sahani ya wali na vinywaji.

Washtakiwa hao walishtakiwa Kinyume na Kifungu cha 97(1)(b) cha Sheria ya Usimamizi wa Kodi [Sura ya 438 Toleo la 2023], kikisomwa pamoja na Vifungu vya 96 na 97 vya Sheria ya Fedha Na. 6 ya mwaka 2024.

Pia imedaiwa walikamatwa, wakati maofisa wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), wakiwa katika utafiti na upelelezi kuhusiana na utoaji wa risiti za kielektroniki. Ambapo imedaiwa waliagiza chakula na vinywaji ila walipewa risiti za mkono.

Hukumu hiyo, imetolewa leo Mei 8, 2026 na Hakimu Mwandamizi Mohamed Burhani, baada ya washtakiwa kukiri mashtaka mawili kushindwa kutoa risiti za kielektroniki kinyume na sheria za kodi.

Akisoma hukumu hiyo, Hakimu Burhani amesema kesi kama hizo lazima adhabu zitolewe ili kuzuia makosa hayo yasitendwe na watu wengine. 

"Kwa mujibu wa sheria sitawapa adhabu ya Magereza nitawaacha huru kwa sababu mmekiri mashtaka yenu, shtaka la kwanza kila mmoja atalipa faini ya Sh milioni mbili na shtaka la pili ambalo linamkabili Fuyu peke yake atalipa Sh milioni mbili." amesema Hakimu Burhani 

Hata hivyo, Hakimu Burhani amewaeleza washtakiwa kuwa wakishindwa kulipa faini hiyo kila mmoja atatumikia kifungo cha miaka mitatu gerezani. 

Hata hivyo washtakiwa waliweza kulipa faini hiyo na kuachiwa huru.

Mapema akisoma hati ya mashtaka Wakili wa Serikali Salome Assey amedai kuwa Machi 24, 2026 katika Mtaa wa Gerezani, eneo la Kariakoo, Wilaya ya Ilala, Mkoa wa Dar es Salaam, wakiwa walitoa huduma za chakula na vinywaji katika Kampuni ya Dicos (Mgahawa wa Kibonge) na kushindwa kutoa risiti ya kielektroniki walipotoa huduma ya chakula ambayo ni sahani moja ya baga yenye thamani ya Sh.13,000.

Katika shtaka la pili, inadaiwa kuwa tarehe hiyo na mahali hapo mshtakiwa Fuyu alishindwa kutoa risiti ya kielektroniki alipotoa huduma ya chakula na vinywaji ambayo ni sahani mbili za chipsi kuku, sahani moja ya wali uliochanganywa na mayai, chupa mbili za plastiki za Coca-Cola na chupa moja ya maji ya kunywa ya Kilimanjaro, vyote vikiwa na thamani ya Shilingi 35,000.

Baada ya washtakiwa kusomewa mashtaka hayo, walikiri kutenda makosa hayo ambayo Hakimu Burhani aliutaka upande wa mashtaka kuwasomea washtakiwa maelezo ya awali (PH).

Alidai kuwa Machi 24,2026 Fuyu akiwa Meneja wa Kampuni hiyo na Mwalutola akiwa mhudumu walikuwa wanatoa huduma ya chakula na vinywaji kwa wateja na tarehe maofisa wa TRA walipewa kazi kwa ajili ya kufanya utafiti na upelelezi katika mgawaha huo kama wanatoa risiti za kielektroniki.

Ilidaiwa kuwa Ofisa wa TRA, Cecilia Lussa aliagiza sahani ya baga ambayo ilikuwa ni Sh. 13,000 na baada ya kulipa fedha alipewa risiti ya mkono, alipouliza kwa nini hajapewa risiti ya kielektroniki aliambiwa mashine haifanyi kazi ni mbovu.

"Na maofisa wengine wawili Hosea Kasiba na Kisabo Focus walifika katika mgawaha huo, wakaagiza sahani mbili za chipsi kuku, sahani moja ya wali iliyochanganywa na mayai, chupa mbili za Coca-Cola na maji ya Kilimanjaro chupa mbili jumla ilikuwa Sh 35,000, baada ya kulipa walipewa risiti ya mkono, walipouliza walielezwa kuwa mashine ni mbovu,"alidai 

Baada ya hapo walijitangaza kama wao ni maofisa wa TRA, watuhumiwa walikwenda kuripoti Idara ya Kodi kwa kosa la kushindwa kutoa risiti za kielektroniki , ambapo walikiri kutenda kosa hilo.

Hata hivyo, washtakiwa walikili maelezo hayo kuwa ni ya kweli, Mahakama ilipokea vielelezo mbalimbali vya Jamhuri ikiwemo risiti walizozitoa kwa wateja kama kielelezo namba moja.

"Baada ya kusomewa mashtaka yenu mmekiri kosa hilo na PH pia mmekiri kutokana na kukiri kwenu Mahakama inawatia hatiani kwa makosa yote. Je! Jamhuri washtakiwa wanamakosa ya nyuma?,"alisema Hakimu Burhani 

Hata hivyo, Wakili Assey alidai hawana taarifa za nyuma za washtakiwa, kwa hiyo hakimu aliwapa nafasi ya washtakiwa kujitetea kabla adhabu haijatolewa.

Fuyu ambaye ni Meneja Kampuni ya Decos Catering Ltd na Mkazi wa GSM Plaza -Gerezani amedai kuwa yeye ni bosi na pia ni mpishi kwa wakati mmoja, kwa hiyo hawezi kuona kinachoendelea kama risiti za kielektroniki zinatolewa au, ila anakubali kutenda kosa hilo.

Mshtakiwa wa pili,  Mwalutola ambaye ni Mkazi wa Temeke Mwembe Yanga alidai kuwa siku hiyo kweli mashine ilikuwa inasumbua ilikuwa ikiandika 'Illegal', lakini ilipotengemaa waliendelea kutoa risiti za kielektroniki kwa sababu ndiyo utaratibu wao ni siku hiyo tu ndiyo kulitokea changamoto. 

Wakati kesi hiyo inaendelea, Mkalimani Maria Katambo alikuwa akitafsiri kutoka lugha ya kiswahili kwenda Kichina na kichina kwenda Kiswahili kwa ajili ya mshtakiwa Fuyu.

Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC), leo tarehe 7 Mei, 2026 limefanya kikao na wadau wa ujenzi wa meli jijini Mwanza kwa lengo la kuhamasisha uwekezaji katika ujenzi wa meli na vyombo vingine vya majini nchini ili kusaidia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Akizungumza wakati alipokutana na ujumbe huo, uliongozwa na Wakili Leticia Mutaki, Mkurugenzi wa Udhibiti, Ulinzi, Usalama na Utunzaji wa Mazingira ya Usafiri Majini, Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mhe. Saidi Mtanda, aliipongeza TASAC kwa kuitisha kikao hicho akisema kuwa kimekuja wakati muafaka kutokana na umuhimu wa sekta ya usafiri majini katika maendeleo ya Mkoa wa Mwanza na Taifa kwa ujumla.

Mhe. Mtanda alisema Mkoa wa Mwanza upo tayari kushirikiana na TASAC katika kuhamasisha uwekezaji kwenye sekta ya ujenzi wa meli kwa kuwa Mwanza ni lango kuu la usafiri majini katika Ukanda wa Ziwa Victoria na kuwa na meli bora kutasaidia kuimarisha usalama wa usafiri majini.

Aliongeza kuwa zaidi ya asilimia 53 ya eneo la Mkoa wa Mwanza ni maji, hali inayodhihirisha umuhimu wa sekta hiyo kwa uchumi wa mkoa.

Kwa upande wake, Wakili Mutaki akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa TASAC alisema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, imeendelea kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji na kuhimiza maendeleo ya uchumi wa buluu pamoja na viwanda vya ndani kupitia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Wakili Mutaki aliongeza kuwa TASAC itaendelea kuhamasisha sekta binafsi kuwekeza katika ujenzi wa meli na vyombo vya majini nchini ili kupunguza utegemezi wa kuagiza vyombo hivyo kutoka nje ya nchi, hatua ambayo pia itasaidia kupunguza matumizi ya fedha za kigeni.

Wadau waliohudhuria kikao hicho ikiwemo kampuni za Songoro Marine, Ankola Shipyard Co. Ltd, na Mkombozi Marine waliishukuru TASAC kwa kuandaa kikao hicho na kueleza kuwa kimewapa fursa ya kutambua maeneo mbalimbali ya uwekezaji katika ujenzi wa meli  pamoja na umuhimu wa kushiriki katika maendeleo ya uchumi wa buluu nchini.













📌Bodi ya Nishati Vijijini (REB)  yafanya kikao na Wakandarasi wa miradi Umeme Vijijini Mkoa wa K'manjaro, Arusha

Bodi ya Nishati Vijijini (REB) ikiongozwa na Mwenyekiti wa Bodi hiyo, Mhe. Balozi Meja Jenerali Mstaafu, Jacob Kingu, leo tarehe 8 Mei, 2026 imefanya kikao na Wakandarasi wanaotekeleza miradi ya kupeleka umeme vijijini katika Mikoa ya Kilimanjaro na Arusha wanaosimamiwa na Wakala wa Nishati Vijijini (REA) ili kupata taarifa ya utekelezani wa miradi hiyo.

Mwenyekiti Kingu ambaye alikuwa ameongozana na Wajumbe wa Bodi hiyo, Mhe. Balozi Radhia Msuya na Mhandisi Sophia Mgonja walikutana na Kampuni ya Ceylex Engineering Limited na Derm Group Limited na ambao wanatekeleza miradi kwa Mkoa wa Kilimanjaro na pia walikutana na Kampuni ya Ceylex Engineering Limited na Nakuroi Investment Company Limited ambazo zinatekeleza miradi kwa Mkoa wa Arusha.

Mwenyekiti Balozi Meja Jenerali Mstaafu Kingu, amewatata wakandarasi hao kutekelezea miradi hiyo ndani ya muda wa mkataba waliosaini na kuhakikisha wanazingatia ubora unaotakiwa.

Kikao hicho ambacho kilihudhuriwa pia na Mkurugenzi wa Umeme Vijijini kutoka REA, Mhandisi Jones Olotu, Meneja Msimamizi wa Miradi kutoka REA, Mhandisi Deogratius Nagu, Meneja wa Teknolojia za Nishati kutoka REA, Mhandisi Michael Kyessi, Mhandisi Miradi kutoka REA, Isaac Sanga pamoja na Mameneja wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) wa Mikoa ya Kilimanjaro na Arusha.









-Azindua Hoteli ya Mikumi Wildlife

-Asema Serikali imetoa sh. bilioni 35 kuboresha uwanja wa Kikoboga, Mikumi


WAZIRI MKUU Dkt Mwigulu Nchemba amewataka watendaji katika taasisi na mamlaka za Serikali wawe tayari kuwawezesha wawekezaji badala ya kuwadhibiti ili wavutiwe kuwekeza zaidi na zaidi.

“Nitoe wito kwa taasisi na mamlaka za Serikali, tumieni muda mwingi kuwawezesha wawekezaji badala ya kuwadhibiti. Washawishini waongeze uwekezaji badala ya kuwafanya waonekane wanaomba. Tumieni vivutio zaidi ili washawishike zaidi na zaidi,” amesema.

Ametoa wito huo leo (Ijumaa, Mei 8, 2026) wakati akizungumza na wadau waliohudhuria uzinduzi wa hoteli ya Mikumi Wildlife katika Hifadhi ya Taifa ya Mikumi, wilayani Kilosa, mkoani Morogoro.

Amesema hoteli hiyo ambayo zamani ilikuwa inamilikiwa na serikali lakini ikapata janga la kuungua moto, ina historia ya miaka mingi; na ana imani na uwekezaji uliofanyika kwani umesaidia kuongeza ajira na kipato kwa wananchi.

“Sina shaka uwekezaji huu utaongeza mvuto kutokana na viwango vilivyopo kwenye hoteli hii. Viwango vya hoteli hii ni vya juu sana, ninaamini vitasaidia kuongeza muda wa watalii kukaa ndani ya hifadhi na uwepo wa malazi mazuri pia utaongeza idadi ya watalii,” amesema.

Akielezea juhudi za serikali kuboresha hifadhi ya Mikumi, Waziri Mkuu amesema Serikali imetoa sh. bilioni 35 za kuboresha uwanja wa ndege wa Kikoboga na ifikapo Oktoba mwaka huu, utakuwa umekamilika.

Amezitaka Wizara ya Maliasili na Utalii, TANAPA washirikiane na mamlaka nyingine za Serikali na kutumia fursa ya stesheni ya Kilosa ili kufungua njia na kuboresha miundombinu itakayorahisisha watalii kuingia katika Hifadhi ya Mikumi na hivyo kuongeza idadi ya watalii.

Ameitaka Wizara ya Maliasili na Utalii iendelee kubuni mikakati ya kwa kuhamasisha sekta binafsi iwekeza katika maeneo ya utalii huku akizitaka taasisi zote za umma ikiwa ni pamoja na mikoa yenye maeneo yaliyo na fursa za utalii ziendelee kuboresha mazingira ya uwekezaji ili kuvutia wawekezaji wengi zaidi. “Suala hili litekelezwe sambamba na kutangaza vivutio vilivyopo.”

Waziri Mkuu amewataka wadau wa utalii waweke mipango ya kuendeleza mazao mapya ya utalii yatakayochochea ongezeko la watalii na kuwahamasisha kuchagua kutembelea vivutio vilivyopo katika Kanda ya Utalii Kusini.

Ametumia fursa hiyo kumwelekeza Waziri wa Maliasili na Utalii aangalie namna ya kuongeza programu za utalii kwenye Chuo cha Ufundi (VETA) kilichopo Mikumi. “Waziri wa Utalii tuongeze programu nyingi za utalii ili vijana wa hapa wanufaike na rasilimali zilizopo katika eneo lao. Kwa maono ya Mheshimiwa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan, alitaka hivi vyuo vinapojengwa viweke programu kulingana na shughuli za kiuchumi za eneo husika kama vile utalii, uvuvi ili viwasaidie vijana wa maeneo husika.”

Mapema, akimkaribisha Waziri Mkuu kuzungumza na washiriki wa hafla hiyo, Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Ashatu Kijaji alisema miaka ya nyuma hifadhi ya Mikumi ilikuwa ikipokea watalii 60,000 kwa mwaka lakini mwaka jana idadi ya watalii iliongezeka sana kufikia 174,808.

“Mapato yanayotokana na utalii yalikuwa sh. milioni 2.5 lakini nayo kwa mwaka jana yaliongezeka na kufikia sh.milioni 9.81. Hadi kufikia tarehe 31 Machi, 2026 idadi ya watalii waliofika kwenye hifadhi ya Taifa ya Mikumi walikuwa 151,275 na mapato yaliyokusanywa yalikuwa yamefikia sh. milioni 10.12,” alisema.

Alisema tayari sh. bilioni nne za kujenga geti upande wa Kilosa zimeshatolewa na ziko hifadhini tayari kuanza kazi hiyo ambapo mtu akishuka Kilosa kwa treni ya SGR atatumia dk.20 tu kuingia hifadhini.

Naye Bw. Simon Nguka, akisoma taarifa kuhusu mradi huo, alisema ujenzi na ukarabati wa hoteli hiyo yenye vyumba 48 na ambayo inamilikiwa na Watanzania kwa asilimia 100, umetumia sh. bilioni 26.8.

Alisema mradi huo ni miongoni mwa miradi 24 waliyonayo. Wellworth Group inamiliki mahoteli, loji, resorts na kambi za kitalii zenye uwekezaji wa thamani ya sh. bilioni 640.







▪️Ateta na WanaGairo, asisitiza kuitunza amani

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amefanya ukaguzi wa daraja la Magole lililopo Dumila katika Mto Mkundi wilayani Kilosa na kuagiza uongozi wa TANROADS utafute suluhu ya kudumu ya changamoto inayolikabili daraja hilo ya kujaa maji na mchanga kila mwaka.

Waziri Mkuu ametoa agizo hilo leo (Ijumaa, Mei 8, 2026) wakati akizungumza na wananchi waliofika darajani hapo kumsikiliza na akamtaka Meneja wa TANROADS Mkoa wa Morogoro ashirikiane na wataalamu wengine kuandaa utaratibu wa kuwaruhusu wananchi kuchimba mchanga katika eneo hilo kwa kuzingatia maelekezo ya kitaalamu, ili kusaidia kupunguza mzigo wa gharama za Serikali na wakati huohuo kulinda miundombinu ya daraja hilo.

“Meneja wa TANROADS na wenzako wote ratibuni eneo ambalo tunahangaika kutoa mchanga na hatuna bajeti, wananchi muwaruhusu watoe mchanga huo kwa utaratibu wa kitaalamu,” amesisitiza Waziri Mkuu.

Akitoa taarifa kuhusu hali ya eneo hilo, Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Adam Malima amesema kuwa kwa muda mrefu daraja hilo limekuwa likikumbwa na changamoto ya kurundikana kwa mchanga unaosababishwa na mtiririko mkubwa wa maji katika mto huo, hali inayohatarisha usalama, ustawi na uimara wa daraja hilo.

Ameeleza kuwa daraja hilo ni la kimkakati linalounganisha Wilaya za Kilosa na Gairo mkoani Morogoro, sambamba na kuwa sehemu ya njia kuu ya usafirishaji wa magari kutoka Dar es Salaam kupitia Morogoro kuelekea Dodoma na mikoa mingine ya nchi.

Kwa mujibu wa Meneja wa TANROADS wa Mkoa huo, Mhandisi Patrick Rambika, Serikali hutumia kati ya sh. milioni 400 hadi 500 kila mwaka kuondoa mchanga unaoziba eneo la daraja hilo ili kuruhusu maji kupita bila kuathiri miundombinu hiyo. Hata hivyo, wakati mwingine upatikanaji wa fedha huwa changamoto na kuongeza hatari kwa uimara wa daraja hilo.

Akiwa eneo la Magoweko, wilayani Gairo, Waziri Mkuu aliwaeleza wananchi juhudi ambazo zimefanywa na Serikali ya awamu ya sita chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan katika sekta za afya, elimu, maji na miundombinu.

Aliwasisitiza wakazi hao watunze amani kwani ndiyo mtaji wa uhai wao. “Gairo kukiwa na amani watu wa kwanza kunufaika ni wanaGairo wenyewe. Kukiwa na uvunjifu wa amani, watu wa kwanza kuathirika ni wanaGairo wenyewe na amani ikipotea inahatarisha uhai wetu.”

“Kila ninakopita ninawakumbushia Watanzania kuwa mtaji wa kwanza wa kufanya shughuli yoyote ni uhai Mungu aliotupatia. Mtaji wa pili wa kufanya shughuli yoyote unayoiwaza ni amani katika eneo lako ulipo.”
















Top News