Kwa mujibu wa taarifa kwa umma iliyotolewa na Mtendaji Mkuu wa TANROADS mapema wiki hii, imeelezwa kuwa taarifa zilizopokelewa zinaonyesha matapeli hao wamekuwa wakiwasiliana kwa njia ya simu na wamiliki wa mabango ya matangazo (billboards), nakujitambulisha kama maafisa wa TANROADS na kudai malipo ili kuzuia kuondolewa kwa mabango yaliyokwisha muda wake.
Taarifa hiyo imeongeza kuwa mbinu zinazotumika na matapeli hao ni pamoja na kutumia lugha ya mamlaka, kutoa vitisho vya kuchukua hatua za kisheria, na kuwaharakisha walengwa kufanya malipo ili kuepuka hatua hizo. Hali hii imekuwa ikiwalenga zaidi wafanyabiashara na wamiliki wa mabango ambao mikataba yao imefikia ukomo.
Kutokana na udanganyifu huo, baadhi ya wananchi tayari wameathirika kwa kupoteza fedha zao baada ya kutuma malipo kwa namba binafsi walizopewa na matapeli hao. TANROADS imesisitiza kuwa haitoi huduma kwa kupokea malipo kupitia namba binafsi za simu au kwa mtu mmoja mmoja, Badala yake, malipo yote hufanyika kupitia mifumo rasmi ya serikali inayotambulika.
Wananchi wametahadharishwa kuwa makini, kuthibitisha taarifa kabla ya kufanya malipo yoyote, na kuepuka kabisa kutuma fedha kwa mtu yeyote anayewasiliana kwa njia hiyo na kujitambulisha kama mtumishi wa TANROADS bila kufuata taratibu rasmi.
Ameeleza kuwa, TANROADS inaendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi kufuatilia utapeli huo ili kuwabaini wahusika na kuchukua hatua kali za kisheria dhidi yao
Wananchi wote wamehimizwa kutoa taarifa za matukio ya aina hiyo kupitia ofisi za TANROADS zilizo karibu au kwa kutumia njia rasmi za mawasiliano za wakala huo, Ushirikiano wa wananchi unatajwa kuwa muhimu katika kusaidia kukomesha vitendo hivyo vya uhalifu.
TANROADS imeeleza kuwa itaendelea kuchukua hatua madhubuti kulinda maslahi ya wananchi na kuhakikisha huduma zake zinatolewa kwa uwazi, usalama na uadilifu, huku ikiwataka wananchi kuwa sehemu ya mapambano dhidi ya matapeli kwa kutoa taarifa mapema wanapobaini viashiria vya udanganyifu.









































.jpeg)



.jpeg)

