Maelekezo ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba aliyoyatoa wakati wa ziara yake ya kikazi wilayani Ikungi na katika Manispaa ya Singida Juni 27, 2026 ya kusikiliza na kusuluhisha migogoro ya ardhi iliyopo mkoani humo yameanza kutekelezwa leo Juni 30, 2026.

Viongozi na watendaji wa mkoa wa Singida na Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi wakishirikiana na Timu ya Watalaamu kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu walikusanyika kwenye ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa kusuluhisha migogoro ya ardhi ya mamia ya mwananchi waliojitokeza wakiwa na vielelezo mbalimbali.

Akizungumza Mkuu wa wilaya ya Singida alimshukuru Kamishina wa Ardhi, Nathaniel Mathew Nhonge kwa kujitoa kwa moyo kutatua migogoro ya ardhi mkoa wa Singida kama ilivyoelekezwa na Waziri Mkuu.

Zoezi hilo limekadiriwa kuendeshwa kwa siku nne ili kuhakikisha kwamba kila mwananchi aliyejitokeza anasikilizwa na suala lake linafanyiwa kazi.

Mkuuwa Mkoa wa Singida, Halima Dendego, Kamishina wa Ardhi, Nathaniel Mathew Nhonge na Mkuu wa wilaya ya Singida Godwin Gondwe ni miongoni mwa viongozi walioongoza usuluhishi huo.






Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali itaendelea kuimarisha mazingira ya biashara, uwekezaji na viwanda kwa kufanya mageuzi ya sera, sheria, kanuni na mifumo ya utoaji huduma ili kuiwezesha sekta binafsi kuwa mhimili wa ukuaji wa uchumi na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Amesema hayo leo, Jumanne Juni 30, 2026, alipokuwa Mgeni Rasmi katika Kongamano la Biashara na Uwekezaji la Mwaka 2026 lililoandaliwa na Chemba ya Taifa ya Biashara Tanzania (TNCC) katika Hoteli ya Johari Rotana, jijini Dar es Salaam.

Waziri Mkuu amesema Serikali imejipanga kuhama kutoka katika mfumo wa kudhibiti biashara kwenda katika mfumo wa kuwezesha biashara kwa kuendelea kuboresha mazingira ya uwekezaji, kupunguza urasimu, kuimarisha matumizi ya teknolojia na kuongeza ufanisi wa taasisi zinazotoa huduma kwa wafanyabiashara na wawekezaji.

"Ajenda ya sekta binafsi ni ajenda ya Taifa. Hatuwezi kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 bila sekta binafsi yenye nguvu, inayowezeshwa na inayoshirikiana kwa karibu na Serikali," amesema.

Aidha, amesema Serikali itaendelea kupokea na kufanyia kazi mapendekezo ya sekta binafsi yanayolenga kuboresha mazingira ya biashara, kuondoa vikwazo vinavyokwamisha uwekezaji na kuongeza ushindani wa bidhaa na huduma za Tanzania katika masoko ya kikanda na kimataifa.

Waziri Mkuu amesema amani, utulivu na mshikamano wa Taifa ni msingi muhimu wa maendeleo ya uchumi, hivyo kila Mtanzania ana wajibu wa kuendelea kuvilinda ili kuwezesha biashara, uwekezaji na uzalishaji kustawi.

Awali, Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga alisema Serikali inaendelea kujenga mazingira rafiki ya biashara kwa kuimarisha ushirikiano na sekta binafsi, kukuza matumizi ya teknolojia na kuhakikisha taasisi za umma zinafanya kazi kwa mtazamo wa kuwezesha biashara badala ya kuzikwamisha.

Kwa upande wake, Rais wa Chemba ya Taifa ya Biashara Tanzania (TNCC), Bw. Vincent Minja alisema chemba hiyo imeendelea kufanya mageuzi ya kiutawala na kidijitali yanayolenga kuboresha huduma kwa wanachama, kuimarisha uwakilishi wa sekta binafsi na kuongeza ushindani wa biashara za Tanzania.

Katika kongamano hilo, Waziri Mkuu alizindua rasmi Mfumo wa Kidijitali wa Chemba ya Taifa ya Biashara Tanzania, utakaorahisisha utoaji wa huduma mbalimbali za chemba hiyo, ikiwemo usajili wa wanachama, utoaji wa vyeti vya asili ya bidhaa na huduma nyingine za biashara kwa njia ya mtandao.

Aidha, alishuhudia utiaji saini wa hati mbalimbali za makubaliano ya ushirikiano kati ya Chemba ya Taifa ya Biashara Tanzania na taasisi za umma pamoja na sekta binafsi, hatua inayolenga kuimarisha biashara, uwekezaji, utafiti, ubunifu na maendeleo ya sekta binafsi nchini.

Kongamano hilo lilihudhuriwa na viongozi wa Serikali, taasisi za umma, sekta binafsi, washirika wa maendeleo, mabalozi, wawekezaji na wafanyabiashara kutoka ndani na nje ya nchi.







Na Eva Ngowi, WF, Harare - Zimbabwe.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-Maamry Mwamba, ameongoza ujumbe wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Kikao cha Makatibu Wakuu wa Hazina na Maafisa Waandamizi wa Benki Kuu wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), kinachofanyika jijini Harare, Zimbabwe, kikijadili masuala mbalimbali ya ushirikiano wa kifedha, uwekezaji na maendeleo ya kiuchumi katika ukanda huo.

Kikao hicho kimewakutanisha Makatibu Wakuu kutoka nchi wanachama wa SADC, ambapo pamoja na ajenda kuu ya utekelezaji wa Mfuko wa Maendeleo wa Kikanda wa SADC, wajumbe walipitia maendeleo ya Viashiria vya vigezo vya uchumi jumla (Macroeconomic Convergence), Uimarishaji wa Masoko ya Mitaji, pamoja na maendeleo ya Mfumo wa Malipo wa Kikanda wa SADC (SADC-RTGS).

Aidha, Kikao hicho kilijadili mapendekezo ya kutumika kwa njia mbadala za kugharamia Bajeti, programu na miradi mbalimbali ya kikanda, ambazo ni kwa kutumia Tozo ya Bidhaa zinazoingia nchini kutoka Nje ya Afrika (Import Levy) na Tozo ya Utalii (Tourism Levy) ambapo nyingi zilionesha wasiwasi wao wa utekelezaji wa njia hizi kwa kuwa zinakinzana na sheria za nchi wanachama za Mamlaka za Mapato na kupunguza mapato na pia zitaongeza gharama za shughuli za Utalii na kupelekea kushuka kwa Sekta ya Utalii.

Kikao hicho pia kilijadili hatua za kuimarisha uwekezaji na maendeleo ya Mfuko wa Maendeleo wa SADC, mapitio ya utekelezaji wa maamuzi ya mikutano iliyopita, uimarishaji wa usimamizi wa sekta ya fedha, pamoja na mikakati ya kupambana na utakatishaji fedha Haramu na ufadhili wa ugaidi katika ukanda wa SADC.

Katika mjadala wa Mfuko wa Maendeleo wa Kikanda, Tanzania imeendelea kusimamia msimamo wake wa kuunga mkono juhudi za utekezaji wa Mfuko huo, huku ikisisitiza umuhimu wa nchi wanachama kuhakikisha utekelezaji wa maamuzi na maazimio yote yanayofikiwa katika vikao vya SADC ili kuharakisha mchakato wa kusaini, kuridhia na kuanza utekelezaji wake.

Akichangia mjadala huo, Dkt. Mwamba alisema utekelezaji madhubuti wa maamuzi ya kikanda ni msingi muhimu wa kuhakikisha programu na miradi ya SADC inatekelezwa kwa ufanisi na kwa wakati.

Alisema ingawa Mfuko wa Maendeleo wa Kikanda wa SADC unalenga kuongeza upatikanaji wa rasilimali fedha kwa ajili ya kugharamia miradi ya maendeleo, bado kuna changamoto zinazohusiana na uwezo wa nchi wanachama kuchangia, hasa kutokana na tofauti za kiuchumi na vikwazo vya kibajeti vinavyoikabili baadhi ya nchi.

“Utekelezaji wa bajeti, programu na miradi ya maendeleo ya kikanda ni muhimu kwa nchi wanachama kuendelea kutekeleza maamuzi na maelekezo yanayotokana na maazimio ya kikao na mikutano mbalimbali ya SADC ili kuharakisha mchakato wa kusaini, kuridhia na kuanza kutekeleza Mfuko huu.” Alisema Dkt. Mwamba

Aidha, alisisitiza umuhimu wa kuzingatia uwezo halisi wa kifedha wa nchi wanachama, akieleza kuwa mchakato wa uanzishaji wa mfuko huo unapaswa kuambatana na tathmini ya kina ya uwezo wa nchi kuchangia mtaji wake, hasa katika mazingira ya ongezeko la madeni na vikwazo vya bajeti.

“Mchakato wa kutekeleza Mfuko wa Maendeleo wa Kikanda wa SADC unapaswa kuzingatia makadirio halisi ya uwezo wa kifedha pamoja na tathmini ya uwezo wa nchi wanachama kuchangia mtaji wa mfuko huo, hususan katika mazingira ya ongezeko la madeni na vikwazo vya kibajeti,” alifafanua Dkt. Mwamba.

Dkt. Mwamba pia alisisitiza umuhimu wa uwiano kati ya michango ya nchi wanachama na rasilimali kutoka kwa washirika wa maendeleo, akibainisha kuwa hatua hiyo ni muhimu katika kulinda hadhi ya Mfuko, kuimarisha uendelevu wake na kuhakikisha unatimiza malengo ya maendeleo ya kikanda.

“Ni muhimu kuzingatia uwiano unaofaa kati ya michango ya nchi wanachama na rasilimali kutoka kwa washirika wa maendeleo. Hii itasaidia kuhifadhi hadhi ya mfuko, kulinda uhuru wake na kufikia vipaumbele vya maendeleo kama ilivyokusudiwa,” aliongeza.

Alihitimisha mchango wake kwa kueleza dhamira ya Tanzania katika mchakato huo, akibainisha kuwa Tanzania tayari imesaini mkataba wa kuanzishwa kwa Mfuko wa Maendeleo wa Kikanda wa SADC, na taratibu za uridhiaji zinaendelea kukamilishwa kabla ya taarifa rasmi kuwasilishwa Sekretarieti ya SADC.

Mapendekezo yanayotokana na kikao hicho yanatarajiwa kuwasilishwa katika Mkutano wa Mawaziri wa Fedha na Uwekezaji wa SADC kwa ajili ya maamuzi yatakayochochea ukuaji wa uchumi, uwekezaji na ushirikiano wa kifedha katika ukanda wa Kusini mwa Afrika.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-Maamry Mwamba, akichangia hoja wakati wa Kikao cha Makatibu Wakuu wa Hazina na Maafisa Waandamizi wa Benki Kuu wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), kinachoendelea jijini Harare, Zimbabwe, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya Mkutano wa Mawaziri wa Fedha na Uwekezaji wa SADC.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-Maamry Mwamba, akifuatilia na kusikiliza hoja mbalimbali zinazowasilishwa na wajumbe wakati wa Kikao cha Makatibu Wakuu wa Hazina na Maafisa Waandamizi wa Benki Kuu wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), kinachoendelea jijini Harare, Zimbabwe.

Viongozi wa mjadala katika mkutano wa ngazi ya juu wa Makatibu Wakuu wa Hazina na Maafisa Waandamizi wa Benki Kuu wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), (kutoka kushoto) ni Mkurugenzi Mkuu Mwandamizi wa Masuala ya Uchumi kutoka Wizara ya Fedha ya Zimbabwe Mhe. Joseph Mverecha, akifuatiwa na Mkurugenzi Mkuu Mwandamizi na Mwenyekiti wa Maafisa Wakuu wa Hazina wa Jamhuri ya Afrika Kusini, Mhe. Themba Zulu, Naibu Katibu Mtendaji anayeshughulikia Ujumuishaji wa Kikanda, Sekretarieti ya SADC Bi. Angele Makombo N’tumba na Mkurugenzi wa Fedha, Uwekezaji na Forodha wa SADC. Dkt. Yolanda Sabino.


Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-Maamry Mwamba, (wanne kushoto) katika picha ya pamoja na Makatibu Wakuu wa Hazina na Maafisa Waandamizi wa Benki Kuu wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), mara baada ya kuhitimishwa kwa kikao chao kilichofanyika jijini Harare, Zimbabwe.

(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini – Wizara ya Fedha)




Na Janeth Raphael MichuziTv 

📌Mlima Mautia waendelea kuibua msisimko wa kisayansi kutokana na Yoderite adimu

Katika safari ya dunia kugundua maajabu ya asili na historia ya mabadiliko ya sayari, Tanzania imeendelea kujitokeza kama moja ya mataifa yenye hazina adimu za kijiolojia. Mojawapo ya maeneo yanayozidi kuvutia macho ya watafiti na watalii wa kisayansi ni Mlima Mautia uliopo wilayani Kongwa, mkoani Dodoma, unaotajwa kuwa na historia ya kipekee duniani kutokana na uwepo wa madini adimu ya Yoderite.

Kwa mujibu wa wataalamu wa jiolojia kutoka Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST), mlima huo ni miongoni mwa maeneo yenye thamani kubwa ya kisayansi, si tu Tanzania bali pia katika ramani ya jiolojia ya dunia, kutokana na mabadiliko makubwa ya kijiolojia yaliyotokea na kuzaa madini hayo adimu.

Akizungumza na waandishi wa habari wakati wa ziara ya kitaalamu iliyofanyika leo Juni 30, 2026, Meneja wa Idara ya Jiolojia wa GST, Maswi Solomoni, amesema Mlima Mautia unatoa ushahidi hai wa historia ya mabadiliko ya tabaka la dunia kupitia miamba na madini yaliyomo ndani yake.

Amefafanua kuwa madini ya Yoderite yaligunduliwa kwa mara ya kwanza mwaka 1959 na mtaalamu wa jiolojia kutoka Marekani, Hatten Yoder, ambaye baadaye jina lake lilitumika kuyatambulisha madini hayo kama heshima kwa mchango wake mkubwa katika tafiti za kisayansi.

“Baada ya kugunduliwa Tanzania mwaka 1959, madini haya yaliaminika kuwa ya kipekee duniani kwa muda mrefu, hadi mwaka 1998 yalipogunduliwa tena katika ukanda wa Zambezi nchini Zimbabwe,” alisema Solomoni.

Kwa mujibu wake, ugunduzi huo wa awali umeifanya Tanzania kutambulika kimataifa kama sehemu ya mwanzo kabisa ambapo madini ya Yoderite yalipatikana, jambo linaloongeza hadhi ya taifa katika ramani ya utafiti wa jiolojia duniani.

Solomoni alisisitiza kuwa Mlima Mautia una uwezo mkubwa wa kuwa kituo muhimu cha utalii wa jiolojia (geotourism), ambapo watafiti, wanafunzi wa sayansi ya ardhi, wanajiolojia pamoja na watalii kutoka sehemu mbalimbali duniani wanaweza kuutembelea kujifunza historia ya malezi ya dunia kupitia miamba yake ya kipekee.

Amebainisha kuwa muundo na historia ya kijiolojia ya mlima huo haujafananishwa na maeneo mengi duniani, jambo linaloufanya kuwa kama “maabara ya asili” kwa tafiti za kisayansi na elimu ya jiolojia.

Wataalamu wanaamini kuwa iwapo kutakuwa na uwekezaji wa kutosha katika uhifadhi, utafiti na utangazaji wa Mlima Mautia, Tanzania inaweza kujijengea nafasi kubwa kama moja ya vituo vinavyoongoza barani Afrika katika utalii wa jiolojia, huku sekta hiyo ikichangia zaidi katika kukuza uchumi wa taifa kupitia utalii wa kisayansi.




 

 Na Janeth Raphael MichuziTv


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema mafanikio ya utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050 yatategemea uwepo wa taasisi za umma zenye ushindani, zinazoendeshwa kwa matumizi ya teknolojia na zinazopimwa kwa matokeo halisi ya utendaji badala ya mazoea ya kazi.

Rais Samia ametoa kauli hiyo leo wakati akizungumza katika hafla ya kupokea gawio kutoka kwa taasisi na mashirika ya umma iliyofanyika Ikulu, Dar es Salaam.

Amesema Dira ya Taifa 2050 inalenga kujenga uchumi imara na shindani, hivyo ni muhimu taasisi za umma zisimamie kwa ufanisi rasilimali za taifa ili ziwe chachu ya maendeleo na kuboresha maisha ya wananchi.

Kwa mujibu wa Rais Samia, mafanikio ya dira hiyo hayatatokana na uwepo wa sera pekee, bali yatategemea namna taasisi zinavyosimamia mitaji ya umma, kupunguza upotevu wa mali na kutumia rasilimali zilizopo kuzalisha fursa mpya za kiuchumi.

"Hatutaweza kujenga uchumi shindani kwa taasisi zinazofanya kazi kwa mazoea. Tunahitaji taasisi zinazopimwa kwa matokeo badala ya takwimu," alisema Rais Samia.

Amesisitiza kuwa Serikali inalenga kuwa na taasisi zinazowajibika, zenye uwezo wa kutumia teknolojia kuongeza ufanisi wa huduma, pamoja na kufungua nafasi zaidi za ushirikiano kati ya sekta ya umma na sekta binafsi kupitia ubia wenye manufaa kwa pande zote.

Rais Samia pia amezitaka taasisi zote za umma kuhakikisha mipango yao ya kimkakati na utekelezaji wa shughuli za kila siku vinaendana na vipaumbele vya Dira ya Taifa 2050, ili malengo yaliyowekwa yaweze kufikiwa na kutoa matokeo yanayoonekana kwa wananchi.

Aidha, ameeleza kuwa ubia kati ya Serikali na sekta binafsi unapaswa kuwa na manufaa kwa wadau wote, huku akisisitiza umuhimu wa Watanzania kunufaika moja kwa moja na fursa zinazotokana na miradi ya maendeleo inayotekelezwa kupitia ushirikiano huo.

Katika hatua nyingine, Rais Samia ametoa wito kwa taasisi na mashirika ya umma kuendelea kuimarisha utawala bora, uwajibikaji na usimamizi madhubuti wa rasilimali za umma ili kuongeza mchango wake katika ukuaji wa uchumi na kufanikisha azma ya Tanzania ya kufikia maendeleo endelevu kupitia Dira ya Taifa 2050.



BENKI ya NMB imetunukiwa tuzo ya mchangiaji bora wa gawio baada ya kuikabidhi Serikali Sh96.9 bilioni, ikiwa ni utambuzi wa mchango wake katika kuongeza mapato ya Taifa na kuchochea utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Tuzo hiyo ilitolewa na Rais Samia Suluhu Hassan katika hafla iliyofanyika Ikulu, Dar es Salaam, Jumanne, Juni 30, 2026.

NMB iliwakilishwa na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi, CPA David Carol Nchimbi, pamoja na Mkurugenzi Mtendaji na Afisa Mtendaji Mkuu, Ruth Zaipuna.

NMB ni miongoni mwa taasisi zilizotoa mchango mkubwa kwa Serikali kupitia gawio, kodi na malipo mengine ya kisheria. Hadi Juni 29, 2026, Serikali ilikuwa imekusanya Sh1.32 trilioni kutoka taasisi na mashirika mbalimbali, huku Sh800 bilioni—sawa na asilimia 60—ikitokana na gawio kutoka taasisi zilizopata faida.

Makusanyo hayo yameongezeka kwa Sh300 bilioni, sawa na asilimia 30, kutoka Sh1.02 trilioni zilizokusanywa Juni mwaka jana. Tuzo hiyo inaipa NMB nafasi ya kipekee miongoni mwa taasisi zinazotafsiri ukuaji wa biashara kuwa manufaa ya moja kwa moja kwa Serikali, wananchi na maendeleo ya Taifa.










 

Habari njema kwa watumiaji wa mafuta nchini. Kuanzia Jumatano, tarehe 01 Julai 2026, bei kikomo za bidhaa za petroli zimeshuka kutokana na kupungua kwa bei za mafuta katika soko la dunia.

Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA), katika kutekeleza majukumu yake kwa mujibu wa sheria, imesema kutokana na kushuka kwa bei za mafuta katika soko la dunia, bei za mafuta katika soko la hapa nchini zinashuka kwa Shilingi 96 kwa lita ya petroli, Shilingi 151 kwa lita ya dizeli na Shilingi 242 kwa lita ya mafuta ya taa.  

Kushuka huku kunatokana na mabadiliko katika soko la dunia, ikiwemo makubaliano yaliyofikiwa hivi karibuni kati ya Marekani na Iran kuhusu vita inayoendelea eneo la Mashariki ya Kati, pamoja na kuruhusu meli za mafuta kupita katika Mlango Bahari wa Hormuz. Hatua hizo zimechangia kupunguza ugumu katika usafirishaji na upatikanaji wa mafuta duniani.

Hata hivyo, wastani wa bei katika soko la dunia bado haujarejea katika kiwango kilichokuwepo kabla ya kuanza kwa vita hiyo tarehe 28 Februari 2026.

 

Equity Group imeongoza na kuandaa ziara ya Biashara na Uwekezaji wa siku nne nchini Tanzania Bara na Zanzibar kuanzia tarehe 29 Juni hadi 2 Julai 2026, ukiwaleta pamoja wawekezaji, wafanyabiashara na viongozi wa biashara kutoka nchi mbalimbali barani Afrika na kwingineko. 

Msafara huo umebuniwa kuonesha fursa za biashara na uwekezaji zilizopo Tanzania, ikiwa ni moja ya chumi zinazokua kwa kasi zaidi Afrika Mashariki, huku ukilenga kuimarisha ushirikiano wa kibiashara na kufungua milango mipya ya uwekezaji.

Kama sehemu ya ziara hiyo, Equity Group iliandaa Kongamano la Biashara katika Ukumbi wa Mfalme, kwenye viwanja vya Maonesho ya Sabasaba, kwa ushirikiano na Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TanTrade). 

Kongamano hilo liliwakutanisha wawekezaji wa kimataifa na biashara za ndani, pamoja na kuwezesha majadiliano kati ya sekta binafsi na Serikali kuhusu fursa za biashara, uwekezaji na ukuaji wa viwanda. 

Mgeni rasmi, Mkurugenzi wa Maendeleo ya Biashara kutoka Wizara ya Viwanda na Biashara, Bw. Sempeho Manongi, alisisitiza dhamira ya Serikali ya Tanzania katika kuweka mazingira wezeshi kwa sekta binafsi, biashara na uwekezaji, sambamba na ajenda ya taifa ya ukuaji wa viwanda na biashara ya kikanda.

Akizungumza katika kongamano hilo, Mkuu wa Wateja Wadogo, wa Kati na Binafsi wa Equity Bank Tanzania, Bi. Theresia Mayanie, alisema Equity inaendelea kuwa daraja muhimu kati ya mitaji na fursa kwa kuwaunganisha wawekezaji na biashara za ndani kupitia huduma za ushauri, fedha za biashara, kubadilisha fedha na mwongozo wa kisheria. 

Naye Mkurugenzi wa Mahusiano ya Biashara wa Equity Group, Bw. AQ Hamza, alieleza kuwa misafara ya biashara ina mchango mkubwa katika kukuza uchumi, kujenga mahusiano ya kibiashara na kuwezesha biashara za kimataifa. 

Aidha, Mkurugenzi wa Ukuzaji wa Biashara wa TanTrade, Bw. Jonathan Nkwabi, aliwasilisha fursa mbalimbali za biashara na uwekezaji nchini Tanzania, kabla ya wawekezaji hao kutembelea maonesho ya Sabasaba na kujionea sekta mbalimbali za biashara na uzalishaji.





















The Rotary Club of Dar es Salaam Oysterbay today donated sanitary pads to female students at the Don Bosco Vocational Training Centre as part of its continued commitment to promoting girls' education, health, and dignity.

The donation, valued at approximately TZS 2 million, comprises 72 cartons containing a total of 1,728 packs. 

Financed through the Club’s community project funds, it will help cover the Centre’s annual sanitary pad needs and ensure that menstruation does not become a barrier to learning, attendance, or participation in vocational education.

The handover took place following the Club's weekly fellowship meeting and brought together Rotary  members, representatives from Don Bosco Vocational Training Centre led by Father Felix, the Centre's Marketing Manager Ms. Sia, and student beneficiaries.

Speaking during the handover, representatives of the Rotary Club of Dar es Salaam Oysterbay emphasized that menstrual health is an important aspect of girls' wellbeing and educational success.

"Every girl deserves the opportunity to pursue her education with confidence and dignity. 


By supporting 

menstrual health, we are helping young women remain in school, participate fully in their studies, and build brighter futures."

Across Tanzania, many girls continue to face challenges accessing menstrual hygiene products, resulting in missed classes and reduced educational opportunities.

 Through this initiative, Rotary seeks to contribute to a future where no girl is disadvantaged because of her monthly cycle.

Father Felix expressed appreciation for the Club's support, noting that partnerships between educational  institutions and community organizations play a vital role in creating an enabling environment where young people can thrive.

The sanitary pad donation marks one of the Rotary Club of Dar es Salaam Oyster Bay’s final community service activities for the 2025–2026 Rotary year, reflecting the Club's ongoing commitment to creating lasting impact through practical, community-driven initiatives.

Rotary International is a global network of volunteers dedicated to solving real-world challenges through service, leadership, and partnerships.

The Rotary Club of Dar es Salaam Oysterbay continues to implement projects that improve health, education.





Na Mwandishi Maalumu, Dar es Salaam

Tanzania imesisitiza umuhimu wa zao la tumbaku kwa uchumi wa nchi kubwa zinazolizalisha barani Afrika, ikitoa wito wa kuimarishwa kwa ushirikiano wa kikanda ili kulinda maisha ya mamilioni ya wakulima na kuhakikisha sera za kimataifa kuhusu tumbaku zinazingatia hali halisi ya nchi zinazozalisha zao hilo.

Akifungua mkutano wa nchi zinazolima tumbaku uliofanyika jijini Dar es Salaam
mwishoni mwa wiki, Waziri wa Kilimo, Daniel Chongolo, alisema tumbaku inaendelea kuwa zao muhimu la kimkakati kutokana na mchango wake mkubwa katika upatikanaji wa fedha za kigeni, ajira, mapato ya Serikali, maendeleo ya viwanda na kupunguza umaskini.

"Kwa nchi zetu, tumbaku si zao la kawaida bali ni bidhaa ya kimkakati inayochangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya uchumi," alisema Chongolo, akisisitiza kuwa sera za kimataifa zinazoihusu sekta hiyo zinapaswa kuzingatia ushahidi wa kisayansi na tathmini halisi ya athari zake kiuchumi na kijamii kwa nchi zinazozalisha.

Alisema tumbaku ni miongoni mwa mazao makuu ya biashara nchini Tanzania, likiwa chanzo cha kipato kwa maelfu ya familia za wakulima, kichocheo cha maendeleo ya maeneo ya vijijini na msingi wa ukuaji wa viwanda vinavyoongeza thamani ya mazao.

Chongolo alisema kupitia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, sekta ya kilimo itaendelea kuwa nguzo ya mageuzi ya uchumi, huku mazao ya kimkakati kama tumbaku yakitarajiwa kuongeza mapato ya mauzo ya nje, ajira na ukuaji wa viwanda.

Aliongeza kuwa zaidi ya wakulima 120,000 waliosajiliwa nchini wanategemea tumbaku moja kwa moja, huku mamia ya maelfu ya wananchi wengine wakinufaika kupitia shughuli za usafirishaji, uchakataji na biashara ya zao hilo.

Katika msimu wa mauzo wa 2024/25, alisema wakulima waliuza kilo milioni 160.9 za tumbaku na kujipatia zaidi ya dola za Marekani milioni 411, jambo linalodhihirisha mchango mkubwa wa zao hilo katika kuongeza kipato cha wakulima na mapato ya fedha za kigeni.

Chongolo alisema umuhimu wa tumbaku hauishii Tanzania pekee, akitolea mfano Malawi ambako zao hilo huchangia takribani asilimia 50 ya mapato yote ya fedha za kigeni, hali inayoonyesha nafasi yake muhimu katika uchumi na maisha ya wananchi wa nchi kadhaa za Afrika.

Alizitaka nchi zinazozalisha tumbaku kuimarisha ushirikiano katika tafiti, matumizi ya teknolojia, kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi, kuongeza thamani ya mazao na kuendeleza uzalishaji endelevu ili kuongeza ushindani katika soko la dunia.

Aidha, alisisitiza umuhimu wa kuwawezesha wakulima wadogo kupitia upatikanaji wa mitaji, huduma za ugani na masoko, huku akizitaka nchi wanachama kuunganisha nguvu katika kutetea maslahi yao ya pamoja kimataifa.

Mwenyekiti wa Bodi ya Tumbaku Tanzania (TTB), Victor Mwambalaswa, alisema mafanikio ya sekta hiyo yanategemea ustawi wa wakulima wa tumbaku.

"Kiini cha juhudi zetu zote ni mkulima wa tumbaku. Maendeleo na uendelevu wa sekta hii yanategemea ustawi wa wakulima wetu," alisema.

Mwambalaswa alisema mkutano huo ni fursa muhimu ya kubadilishana uzoefu, kutafuta suluhisho la changamoto zinazokabili sekta hiyo na kuimarisha ushirikiano katika mnyororo mzima wa thamani wa tumbaku.

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu wa Idara ya Uchambuzi wa Sera, Uratibu, Ugatuzi na Mipango ya Maendeleo katika Ofisi ya Rais na Baraza la Mawaziri la Zimbabwe, Dk. Willard Manungo, alisema tumbaku ni moja ya nguzo kuu za uchumi wa nchi yake.

Alisema Zimbabwe inalenga kuvuna kilo milioni 400 za tumbaku mwaka 2026 kutoka kilo milioni 355 zilizovunwa mwaka 2025, huku sekta hiyo ikiwaingizia wakulima zaidi ya dola za Marekani bilioni 1.2 mwaka uliopita.

Aliongeza kuwa zaidi ya kaya 135,000 nchini humo zinategemea kilimo cha tumbaku kwa maisha yao, huku Serikali ikitekeleza awamu ya pili ya Mpango wa Maboresho wa Mnyororo wa Thamani wa Tumbaku (2026–2030), unaolenga kuongeza uzalishaji hadi kilo milioni 500, kukuza uchakataji wa ndani, kuongeza thamani ya zao na kuimarisha ushindani katika soko la kimataifa.

Dk. Manungo alisema Zimbabwe pia inawekeza katika uhifadhi wa mazingira kupitia upandaji miti, matumizi ya teknolojia za ukaushaji zinazookoa nishati, kilimo himilivu dhidi ya mabadiliko ya tabianchi na kuimarisha viwango vya kimazingira, kijamii na utawala bora.

Pamoja na changamoto za ziada ya uzalishaji duniani na kushuka kwa bei, alisema ushirikiano wa karibu kati ya nchi zinazozalisha tumbaku ni muhimu ili kuhakikisha sekta hiyo inabaki kuwa endelevu, yenye ushindani na yenye manufaa kwa wakulima.
Waziri wa Kilimo Mheshimiwa Daniel Chongolo akipokelewa na Mwenyekiti wa Bodi ya Tumbaku Victor Mwambalaswa alipowasili kufungua mkutano wa wadau wa tumbaku kutoka kwenye nchi tano za Afrika uliofanyika Dar es Salaam mwishoni mwa juma.
Waziri wa Kilimo Daniel Chongolo ma wadau wa tumbaku akielekea ukumbini kufungua mkutano wa wadau wa tumbaku mara baada ya kuwasili.Katikati ni Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Prof.Peter Msofe na kushoto ni Mkurugenzi wa Bodi ya Tumbaku Stanley Mnozya.
Waziri wa Kilimo Daniel Chongolo akiwa katika picha ya pamoja na wadau wa zao la tumbaku kutoka nchi 5 za Afrika mara baada ya kufungua mkutano wao mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam
Wadau wa zao la tumbaku kutoka nchi tano za Africa wakimsikiliza Waziri wa Kilimo Daniel Chongolo wakati akifungua mkutano wao uliofanyika mwishoni mwa wiki Jijini Dar ea Salaam

 



MERIDIANBET, kupitia programu yake ya Uwajibikaji kwa Jamii (CSR), imeendelea kuthibitisha kuwa mafanikio ya biashara yana maana zaidi yanapoweza kugusa maisha ya watu moja kwa moja. Safari hii, kampuni hiyo imefika katika kata ya Kasekese, Manispaa ya Wilaya ya Tanganyika mkoani Katavi na kutoa msaada wa taulo za kike katika kampeni ya Hedhi Salama, hatua ambayo imepokelewa kwa furaha kubwa na viongozi pamoja na wananchi wa eneo hilo. Msaada huo umebeba ujumbe mkubwa wa matumaini, heshima na uwekezaji katika kizazi cha kesho.

Kwa miaka mingi, changamoto ya upatikanaji wa bidhaa za msingi za usafi imekuwa ikiwakabili wasichana wengi, hasa katika maeneo ya vijijini. Kutokana na hali hiyo, baadhi yao hulazimika kukosa vipindi vya masomo au hata kuathiriwa kisaikolojia kutokana na mazingira yanayowazunguka. Meridianbet imeona umuhimu wa kushiriki katika kampeni hii ya Hedhi Salama hili kuhakikisha kuwa wasichana wanapata mahitaji muhimu yanayowasaidia kuendelea na masomo yao kwa kujiamini zaidi.

Meridianbet haikuachi nyuma, kuna michezo mbalimbali ya kasino mtandaoni pamoja na mechi za kimataifa za kubashiri zenye odds bomba na nafasi ya kuongeza kipato chako kila siku. Kujiunga ni rahisi! Tembelea tovuti ya MERIDIANBET au piga *149*10#.

Akizungumza baada ya kupokea msaada huo, Afisa Mtendaji wa Kata ya Kasekese Bi. Bahati Kasanga alieleza kuwa mchango huo umefika kwa wakati muafaka na utaongeza nguvu katika jitihada za kuhakikisha wasichana wanabaki shuleni na kufikia malengo yao ya kielimu. Alisisitiza kuwa msaada wa Meridianbet sio tu umetoa suluhisho la muda mfupi, bali pia umeleta hamasa mpya kwa jamii kuzungumza kwa uwazi kuhusu afya ya hedhi na haki za mtoto wa kike. Kauli hiyo imeungwa mkono na wadau mbalimbali ambao wamepongeza hatua ya kampuni hiyo kuwekeza katika maisha ya vijana.

Kwa upande wake, Meridianbet imeendelea kusisitiza kuwa dhamira yake ni kuwa zaidi ya kampuni ya burudani, ni kuwa mshirika wa maendeleo ya jamii. Kupitia miradi yake ya kijamii inayotekelezwa katika maeneo mbalimbali nchini, kampuni hiyo imekuwa ikilenga kugusa maisha ya wananchi kwa njia zinazozalisha matokeo chanya ya muda mrefu. Msaada huu wa taulo za kike ni sehemu ya maono mapana ya kuhakikisha kuwa kila msichana anapata nafasi sawa ya kufanikiwa bila kuzuiwa na changamoto zinazoweza kutatulika.

Katika kipindi ambacho vijana ndio nguvu kazi na tumaini la taifa, Meridianbet inaamini kuwa kila hatua inayochukuliwa leo inaweza kubadilisha maisha ya kesho. Kupitia msaada huu kwa wasichana wa Wilaya ya Tanganyika, kampuni hiyo imeonyesha kuwa uwajibikaji kwa jamii sio kauli mbiu pekee, bali ni ahadi ya kweli ya kushiriki katika kujenga Tanzania yenye usawa, afya bora na fursa kwa kila kijana.

Top News