Dar es Salaam — Kampuni ya michezo ya kubashiri ya PigaBet imetangaza rasmi kuingia mkataba wa udhamini na klabu ya Fountain Gate FC wenye thamani ya Shilingi bilioni 1, hatua inayotarajiwa kuongeza nguvu katika maendeleo ya soka nchini Tanzania.

Ushirikiano huo umetangazwa jijini Dar es Salaam, ukiwa ni sehemu ya mkakati wa PigaBet kuendeleza michezo kama chachu ya mshikamano wa jamii, ukuaji wa uchumi na kuinua hadhi ya taifa kupitia soka.

Hatua hiyo pia inaenda sambamba na mwanzo wa enzi mpya kwa Fountain Gate FC, ambayo sasa imehamishia makazi yake jijini Arusha, eneo linalozidi kujijenga kama kitovu cha michezo nchini kuelekea michuano ya Africa Cup of Nations 2027.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Meneja wa Masoko wa PigaBet, Arthur Kazola, alisema kampuni hiyo inaamini nguvu ya soka katika kuunganisha jamii na kuhamasisha vijana.

“Ushirikiano wetu na Fountain Gate FC si udhamini wa kawaida, bali ni uwekezaji katika mustakabali wa mpira wa miguu na kuinua hadhi ya Arusha kama jiji la michezo,” alisema Kazola.

Aliongeza kuwa Tanzania inaendelea kujijengea heshima barani Afrika katika soka, hivyo ni muhimu kwa sekta binafsi kuunga mkono juhudi hizo kwa vitendo.

Kwa upande wake, Rais wa klabu hiyo, Japhet Makau, alisema ujio wa PigaBet ni hatua kubwa si kwa klabu pekee bali kwa maendeleo ya soka la Tanzania kwa ujumla.

“Uwekezaji huu unaonesha wazi kuwa soka limekuwa chanzo cha ajira na fursa kwa vijana wetu. Tunakaribisha wadau wengine kuja kuunga mkono juhudi hizi,” alisema Makau.

Kwa mujibu wa makubaliano hayo, PigaBet itashiriki katika kusaidia maendeleo ya klabu ndani na nje ya uwanja, ikiwa ni pamoja na kuimarisha uhusiano na mashabiki na wadau wa soka.

Ushirikiano huo utaanza kuonekana rasmi Aprili 9, 2026, ambapo Fountain Gate FC itakuwa mwenyeji wa Simba SC katika Uwanja wa Sheikh Amri Abeid Stadium, katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara unaotarajiwa kuvuta hisia za mashabiki wengi.

Kwa ujumla, hatua hii inaonekana kuwa kichocheo kipya cha maendeleo ya soka nchini, huku Arusha ikiendelea kujipambanua kama jiji muhimu katika ramani ya michezo Tanzania.











DODOMA, 2 Aprili 2026 

Kuelekea sikukuu ya Pasaka, Meneja wa TRA Mkoa wa Dodoma, Bw. Pendolake Elinisafi, ameongoza ziara ya kutembelea kaya za watu wenye ulemavu wa macho wilayani Chamwino (Matembebora), akiongozana na Meneja Msaidizi Huduma kwa Walipa Kodi, Bw. John Njau, pamoja na watumishi wengine wa TRA Mkoa wa Dodoma, kwa lengo la kutoa faraja, upendo na kuwajengea matumaini, akisisitiza kuwa wao ni sehemu muhimu ya jamii inayothaminiwa.

Akizungumza kwa niaba ya wanakaya hao, Mwenyekiti Bw. Yeledi Cheleso ameishukuru TRA Dodoma kwa moyo wa kujali na msaada walioutoa, akieleza kuwa hatua hiyo imeongeza faraja na kuwapa nguvu mpya ya kuendelea na maisha.

Kwa upande wake, Afisa Maendeleo ya Jamii, Bi. Elizabeth, ameipongeza TRA kwa kuendeleza mshikamano na jamii, akibainisha kuwa juhudi hizo zinaimarisha ushirikiano kati ya taasisi na wananchi, hususan kwa makundi yenye uhitaji maalum.

Ziara hiyo imeacha ujumbe wa upendo na mshikamano, ikionesha dhamira ya TRA ya kuendelea kugusa maisha ya jamii sambamba na majukumu yake ya ukusanyaji wa mapato. 











Na Mwandishi wa OMH

Dar es Salaam. Ofisi ya Msajili wa Hazina (OMH) imeanza zoezi la uchambuzi wa mipango na bajeti za taasisi na mashirika ya umma, likilenga kuimarisha mchango wa taasisi hizo katika utekelezaji wa Dira 2050.

Akizungumza kuhusu zoezi hilo, Alhamis, Aprili 2, 2026, Bw. Joseph Mwaisemba, Mkurugenzi Msaidizi wa Tathmini ya Mashirika yasiyo ya kibiashara (kwa upande wa mamlaka za udhibiti), alisema jumla ya watumishi 50 wa OMH wamekutana katika Shule ya Uongozi ya Mwalimu Nyerere kwa ajili ya kuchambua bajeti za taasisi na mashirika ya umma 252.

Alisema uchambuzi huo unalenga kuangalia namna taasisi hizo zilivyojipanga katika kutekeleza Dira 2050 sambamba na Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano (FYDP IV).

“Tunachofanya hapa ni kuangalia kwa kina mipango ya taasisi na mashirika ya umma ili kuona namna inavyochangia utekelezaji wa Dira 2050 na mipango ya maendeleo ya taifa kwa ujumla,” alisema.

Aidha, alieleza kuwa zoezi hilo pia linahusisha uchambuzi wa mikakati ya taasisi hizo katika kutafuta rasilimali fedha kwa ajili ya kutekeleza bajeti ya mwaka wa fedha 2026/27.

Kwa mujibu wake, OMH inasimamia jumla ya taasisi 308, kati ya hizo 252 zinamilikiwa na serikali kwa hisa nyingi na 56 zinamilikiwa na serikali kwa hisa chache, huku jumla ya uwekezaji ukiwa ni Sh92.3 trilioni.

OMH pamoja na mashirika yake yaliyo chini yake yanatarajiwa kukusanya Sh1.8 trilioni kama mapato yasiyo ya kodi katika mwaka wa fedha 2026/27, ikiwa ni sehemu ya bajeti ya Serikali inayokadiriwa kufikia Sh62 trilioni.

“Hivyo basi, unaweza kuona namna ambavyo zoezi hili lilivyo muhimu katika kuhakikisha malengo ya Serikali yanafikiwa,” alisisitiza.

Kisheria, utekelezaji wa zoezi hilo la uchambuzi unaongozwa na matakwa ya kifungu cha 10(2)(c) cha Sheria ya Msajili wa Hazina, Sura ya 370, pamoja na kifungu cha 17(a) cha Sheria ya Bajeti, Sura ya 439, vinavyoitaka OMH kufanya uchambuzi wa mipango na bajeti za taasisi na mashirika ya umma yaliyo chini yake.

Kwa kuzingatia msingi huo wa kisheria, lengo la uchambuzi huo ni kuidhinisha mikakati na mipango ya mwaka ya taasisi na mashirika ya umma, na kuijumuisha katika Mpango wa Taifa wa Maendeleo kwa ajili ya usimamizi madhubuti wa utekelezaji pamoja na upatikanaji wa rasilimali za kugharamia mipango hiyo.

Aliongeza kuwa katika uchambuzi huo, wataalamu wanapitia mipango ya matumizi ya rasilimali kwa kuangalia mgawanyo kati ya matumizi ya kawaida, miradi ya maendeleo, pamoja na michango ya taasisi katika bajeti kuu ya Serikali.

Maeneo makuu yanayopewa kipaumbele ni pamoja na tathmini ya namna taasisi zilivyojipanga kutekeleza miradi ya maendeleo kwa kutumia fedha za Serikali na zile zinazotokana na vyanzo vya ndani vya mashirika husika.

Baada ya kukamilika kwa uchambuzi huo, bajeti zitaingizwa katika mfumo wa mipango na bajeti wa Serikali (PlanRep), kabla ya OMH kuendelea na jukumu la kufuatilia utekelezaji wake kwa kila robo mwaka ili kuhakikisha malengo yaliyokubaliwa yanafikiwa.

Bw. Mwaisemba alitoa wito kwa taasisi na mashirika ya umma kushirikiana kikamilifu katika kuhakikisha rasilimali chache zilizopo zinatumika kwa ufanisi katika upangaji na usimamizi wa mipango.

“Ufanisi wa kila shirika katika kutekeleza majukumu yake utaakisi moja kwa moja mafanikio ya utekelezaji wa Dira 2050 pamoja na mipango ya maendeleo ya taifa,” alisisitiza.









 

Na.Mwandishi Wetu

TUME ya Ushindani (FCC) Kanda ya Nyanda za Juu Kusini imeadhimisha Wiki ya Haki za Mlaji Duniani kwa kutoa msaada wa vifaa tiba katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda Mbeya, ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za kuboresha huduma za afya kwa wananchi.

Shughuli hiyo imefanyika tarehe 31 Machi, 2026 ambapo FCC imekabidhi vifaa tiba vinne vya Oxygen Flow Meter vitakavyosaidia wagonjwa wanaohitaji huduma ya hewa tiba, hususan wale wanaopata changamoto ya kupumua.

Akizungumza wakati wa hafla ya makabidhiano hayo, Mkuu wa FCC Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, Bw.Dickson Mbanga, amesema kuwa tukio hilo ni sehemu ya kuadhimisha Wiki ya Haki za Mlaji Duniani pamoja na kutimiza miaka mitatu tangu kuanzishwa kwa ofisi hiyo katika ukanda huo.

Mbanga ameeleza kuwa FCC imeona ni vyema kutumia maadhimisho hayo kwa kutoa mchango wa kijamii utakaoleta tija moja kwa moja kwa wananchi, hasa katika sekta ya afya ambayo ni nyeti na muhimu kwa ustawi wa jamii.

 "Vifaa hivyo vitasaidia kuongeza uwezo wa hospitali katika kuhudumia wagonjwa wanaohitaji msaada wa hewa tiba, hivyo kupunguza changamoto zinazoweza kujitokeza wakati wa utoaji wa huduma hizo."amesema Bw.Mbanga

Kwa upande wake, akipokea vifaa hivyo kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Rufaa ya Kanda Mbeya, Muuguzi Kiongozi Ndg. Petro Seme ametoa shukrani za dhati kwa FCC kwa msaada huo muhimu.

Seme amesema kuwa vifaa hivyo ni vya kisasa na vina uwezo wa kuhudumia wagonjwa wawili kwa wakati mmoja, jambo ambalo litarahisisha upatikanaji wa huduma ya hewa tiba na kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma kwa wagonjwa.

Na Mwandishi Wetu

WAFANYABIASHARA na mawakala wa zao la parachichi wilayani Rungwe wamepongeza juhudi za Mamlaka ya Udhibiti wa Nafaka na Mazao Mchanganyiko (COPRA) kwa kuendesha mchakato wa usajili unaolenga kuwatambua rasmi wadau wa sekta hiyo.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti, wafanyabiashara hao wamesema kuwa hatua hiyo ni muhimu katika kuleta utaratibu mzuri wa biashara ya parachichi, hususan kwa kupunguza vitendo vya wizi na ulaghai vilivyokuwa vikifanywa na baadhi ya watu wasiokuwa waaminifu waliojiingiza kwenye biashara hiyo bila utambuzi rasmi.

Aidha, wameeleza kuwa kupitia usajili huo, itakuwa rahisi kwa mamlaka husika kufuatilia mwenendo wa biashara, kulinda maslahi ya wakulima na wafanyabiashara halali, pamoja na kuongeza uaminifu katika soko la zao hilo lenye mchango mkubwa kiuchumi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Nafaka na Mazao Mchanganyiko (COPRA) Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, Bw. Samwel Msuya, amewasisitiza wafanyabiashara na mawakala wa parachichi kuendelea kujisajili ili waweze kunufanya biashara katija utaratibu unaotambulika.

Amesema kuwa usajili huo si kwa wafanyabiashara na mawakala katika wilaya ya Rungwe pekee bali ni kwa mikoa yote inayizalisha parachichi nchini.




Katika jitihada za kuchochea matumizi ya simu janja na kupanua upatikanaji wa huduma za kidijitali, Yas imetambulisha promosheni ya muda mfupi katika kipindi hiki cha Pasaka inayotoa punguzo la bei kwa simu janja za ZTE.

Ofa hiyo ya siku tisa, imeanza rasmi tarehe 31 Machi na itadumu hadi tarehe 8 Aprili. Kupitia promo hiyo, malipo ya awali ya simu za ZTE yameshushwa kutoka Shilingi 45,000 hadi shilingi 25,000. Baada ya hapo, wateja wataendelea kulipia malipo nafuu ya kila siku ya shilingi 950 kwa kipindi cha miezi 12, hatua inayorahisisha zaidi umiliki wa simu janja kwa watanzania wengi.

Kama sehemu ya ofa hii, wateja pia watapata MB 150 za intaneti bure, zitakazowawezesha kuanza mara moja kufurahia mtandao mpana na wenye kasi zaidi nchini (Yas) pamoja na huduma zake za kidijitali.

Akizungumzia promosheni hiyo, Meneja wa Vifaa, Mauzo na Usambazaji - Yas, Bi. Imelda Edward, alisema mpango huo unaakisi dhamira endelevu ya kampuni katika kupunguza pengo la kidijitali nchini.

“Promosheni hii ya Pasaka haihusu tu punguzo la bei. Inalenga kuwawezesha Watanzania wengi zaidi kuingia mtandaoni na kushiriki kikamilifu katika uchumi wa kidijitali. Kwa kutoa punguzo la bei kwenye malipo ya awali na kutambulisha mpango rahisi wa malipo ya kila siku, tunaondoa vikwazo vinavyowazuia Watanzania wengi kumiliki simu janja,” alisema.

Aliongeza kuwa promosheni hiyo inaendana na mkakati mpana wa Yas wa kutoa huduma bora na muunganisho wa kuaminika kote nchini.

“Tunajivunia kutoa mtandao uliotambuliwa kuwa wa kasi zaidi nchini Tanzania na Ookla kwa nyakati tatu mfululizo. Kupitia promosheni hii, tunataka kuhakikisha Watanzania wengi zaidi wanapata fursa ya kujionea ubora wa mtandao wetu kupitia vifaa vya ZTE,” aliongeza.

Promosheni ya Pasaka inatarajiwa kuongeza matumizi ya simu janja, hasa kwa watumiaji wapya, huku ikiendelea kuchochea ukuaji wa mfumo wa kidijitali nchini. Wateja wanahimizwa kutembelea maduka ya Yas na mawakala walioidhinishwa kote nchini ili kunufaika na ofa hii ya muda mfupi kabla ya kumalizika.

Imelda Edward - Meneja wa Vifaa - Mauzo na Usambazaji - Yas Tanzania

 







Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, akisalimiana na Kiongozi Mkuu wa Kanisa Katoliki Duniani, Baba Mtakatifu Leo XIV, mara baada ya Ibada ya Hija iliyofanyika katika Uwanja wa Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro – Vatican, leo tarehe 01 April 2026


Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA) imemkaribisha rasmi Mkurugenzi Mtendaji mpya, CPA Prof. Siasa Issa Mzenzi, katika ofisi za Makao Makuu ya Bodi hiyo jijini Dodoma, Aprili 1, 2026, ikiwa ni hatua ya kuanza rasmi kwa utekelezaji wa majukumu yake.

Akizungumza mara baada ya kuwasili ofisini hapo, CPA Prof. Siasa Issa Mzenzi alisisitiza umuhimu wa ushirikiano kwa wafanyakazi, akibainisha kuwa mafanikio ya Taasisi yoyote yanategemea mshikamano, uwajibikaji na ufanisi wa kila mfanyakazi.

“Ni muhimu kila mmoja wetu akatimiza wajibu wake kwa ufanisi na kwa kuzingatia maadili ya kazi, ili kuendelea kujenga taswira nzuri ya Taasisi,” alisema CPA Prof. Siasa Issa Mzenzi.

Aidha, alitumia fursa hiyo kusikiliza na kupokea kero pamoja na maoni mbalimbali kutoka kwa wafanyakazi, huku akiahidi kuyafanyia kazi kwa lengo la kuboresha mazingira ya utendaji kazi na kuongeza ufanisi ndani ya Taasisi.

Sambamba na hilo, CPA Prof. Siasa Issa Mzenzi alikutana na Mhasibu Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, CPA Leonard Mkude, ofisini kwake jijini Dodoma, kwa lengo la kufahamiana na kuendeleza uhusiano wa kikazi uliopo kati ya ofisi hiyo na NBAA.

Katika mazungumzo yao, CPA Prof. Siasa Issa Mzenzi alisisitiza dhamira ya kushirikiana kwa karibu na serikali pamoja na wadau wa Taaluma ya Uhasibu ili kuhakikisha Taaluma hiyo inaendelea kukua na kufikia viwango vya kimataifa.

“Tutashirikiana na Serikali na wadau mbalimbali wa Taaluma ya Uhasibu kuhakikisha kuwa Taaluma yetu inaendelea kuwa na viwango vya kimataifa, pamoja na kuimarisha uwazi na mawasiliano kwa wananchi,” alisema CPA Prof. Siasa Issa Mzenzi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA), CPA Prof. Siasa Issa Mzenzi akisaini kitabu cha wageni mara baada ya kuwasili katika ofisi za Makao Nakuu ya Bodi hiyo yaliyopo jijini Dodoma.
Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA), CPA Prof. Siasa Issa Mzenzi akizungumza jambo alipokuwa akitembelea ofisi za Bodi hiyo jijini Dodoma.
Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA), CPA Prof. Siasa Issa Mzenzi akizungumza na baadhi ya wafanyakazi wa NBAA alipowasili katika ofisi za Makao Makuu ya Bodi hiyo jijini Dodoma.
Baadhi ya wafanyakazi wa NBAA wakimsikiliza Mkurugenzi Mtendaji wa NBAA, CPA Prof. Siasa Issa Mzenzi alipokuwa akizungumza na wafanyakazi wa Bodi alipowasili katika ofisi za Makao Makuu ya Bodi hiyo jijini Dodoma.
Mhasibu Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, CPA Leonard Mkude akizungumza na Mkurugenzi Mtendaji mpya wa NBAA, CPA Prof. Siasa Issa Mzenzi alipofika kujitambulisha katika ofisi yake jijini Dodoma akisindikizwa na baadhi ya viongozi wa NBAA.
NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

CHUO Kikuu Mzumbe, Ndaki ya Dar es Salaam katika kituo chake cha Tegeta, kimetoa elimu ya uelewa kwa wanawake 200 kuhusu usimamizi wa mirathi, ikiwa ni jitihada za kupunguza migogoro ya kifamilia inayotokana na masuala ya urithi.

Akizungumza Aprili 1, 2026 jijini Dar es Salaam wakati wa semina hiyo, Rasi wa Chuo hicho, Prof. Cyricus Binamungu, amesema mafunzo hayo ni sehemu ya mpango endelevu wa kuwakutanisha wanajamii ili kuwajengea uelewa mpana juu ya masuala ya mirathi.

Amesema usimamizi wa mirathi ni suala nyeti, huku mali nyingi zikibaki katika akaunti za mahakama zikisubiri kuchukuliwa na warithi kutokana na migogoro isiyoisha miongoni mwa familia.

“Unakuta mali nyingi zipo mahakamani zinasubiri warithi, lakini migogoro inapochelewesha taratibu, mali hizo haziwafikii walengwa kwa wakati,” amesema Prof. Binamungu.

Ameongeza kuwa wanaamini elimu hiyo itasaidia kupunguza kwa kiasi kikubwa migogoro hiyo na kuwezesha familia kusimamia vyema urithi wao.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Tegeta, Bered Ntabaliba, amekipongeza chuo hicho kwa kuwafikishia wananchi elimu hiyo muhimu, akieleza kuwa itawasaidia wanawake kujisimamia na kufuatilia masuala ya mirathi kwa ufanisi zaidi.

Amesema eneo la Tegeta limekuwa likikumbwa na migogoro mingi ya mirathi, hivyo semina hiyo itachangia kupunguza changamoto hiyo kwa kuwapa wananchi uelewa wa sheria na taratibu husika.

“Hili ni somo muhimu sana kwetu, litasaidia wananchi kuelewa namna ya kurithi mali na kuepuka migogoro ya kifamilia,” amesema Ntabaliba.

Baadhi ya washiriki wa semina hiyo wameishukuru Mzumbe kwa kuwapatia mafunzo hayo, huku wakitoa wito kwa taasisi nyingine kuendelea kutoa elimu kama hiyo ili kupunguza migogoro inayojitokeza katika jamii, hususan ndani ya familia.
















Top News