Na FARIDA MANGUBE, MOROGORO
Wakati vijana wengi wakikabiliwa na changamoto za maadili na msukumo rika, Serikali imeidhinisha rasmi kitabu cha Dunia Yangu Bora kitakachotumika kufundisha stadi za maisha kwa wanafunzi wa sekondari katika halmashauri 76 za mikoa 10 nchini.
Hatua hiyo inaashiria upanuzi wa utekelezaji wa programu hiyo iliyokuwa ikitumika katika halmashauri 35 pekee kabla ya kuongezwa halmashauri 41 zaidi, na hivyo kufikia jumla ya halmashauri 76.
Mkuu wa Idara ya Miradi kutoka Campaign for Female Education (CAMFED), Bi Dominica Lyambo, amesema kabla ya ithibati rasmi, kitabu hicho kilikuwa kikitumika kwa majaribio katika baadhi ya halmashauri, lakini sasa kitapewa wigo mpana zaidi baada ya kuidhinishwa na Serikali.
Lyambo amesema lengo la kitabu hicho ni kuwajengea wanafunzi uwezo wa kujitambua, kuelewa sababu za kuwa shuleni na namna ya kukabiliana na changamoto za maisha.
“Ni stadi za maisha zinazomsaidia mwanafunzi kuelewa kwa nini yupo shuleni, kwa nini anapaswa kusoma, changamoto zilizopo katika jamii na namna ya kuzikabili ili kufikia ndoto zake,” alisema Lyambo.
Aliongeza kuwa utekelezaji wa programu hiyo unatarajiwa kuongeza mahudhurio ya wanafunzi shuleni na kuboresha kiwango cha ufaulu.
Kwa mujibu wa CAMFED, mpango wao ni kuhakikisha ifikapo mwaka 2030 wanafikia angalau asilimia 85 ya halmashauri zote za wilaya katika mikoa 26 ya Tanzania Bara, kutoka mikoa 10 iliyofikiwa kwa sasa.
Lyambo alisisitiza kuwa programu hiyo inawahusisha wanafunzi wote wa kidato cha kwanza na cha pili wavulana na wasichana na utekelezaji wake utakuwa endelevu.
Katika utekelezaji wake, kila halmashauri imeteua walimu wawili hadi wanne watakaopatiwa mafunzo maalum, kisha kuwafundisha wawezeshaji wengine watakaosimamia mafunzo hayo ngazi ya shule.
Akizungumzia upekee wa kitabu hicho, Lyambo alisema tofauti na vitabu vya masomo ya darasani, Dunia Yangu Bora kinajikita katika ustawi wa binafsi, maadili, uwezo wa kujisimamia na kukabiliana na changamoto za kihisia na kijamii.
Kwa upande wake, Afisa Mwandamizi kutoka Ofisi ya Kamishna wa Elimu, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Fredy Nyandoro, amesema kitabu hicho kimepewa ithibati kama kitabu cha ziada chenye maudhui ya stadi za maisha yanayokamilisha masomo ya kawaida.
Amesema maudhui yake yanawalenga vijana wa Kitanzania walioko katika umri wa balehe kwa kuwajenga katika misingi ya uadilifu, uwajibikaji, kujituma, upendo, utu na utunzaji wa mazingira.
“Dunia ya sasa inawakabili vijana na changamoto nyingi za kuporomoka kwa maadili. Kitabu hiki kinamjenga kijana kuipenda na kuitunza dunia yake, kuelewa mchango wake katika jamii na kushiriki kutatua changamoto,” alisema.
Aliongeza kuwa kitabu hicho kinatumia visa na hadithi zinazoonesha namna ya kushirikiana na wazazi, marafiki na jamii katika kutatua changamoto, huku kikisisitiza kuwa hakuna kukata tamaa katika maisha.
Akizundua kitabu hicho Mwakilishi wa Kamishna wa Elimu nchini, Dkt. Gladness Kirei, amezitaka halmashauri 76 zilizoanza kutekeleza programu hiyo kuwa na mpango kazi madhubuti wa kuhakikisha elimu ya stadi za maisha inatekelezwa kikamilifu mashuleni.
Pia amewataka maafisa elimu kata kufuatilia utekelezaji wake kwa kukusanya takwimu za mahudhurio na kufanya tathmini ya ufundishaji, huku akisisitiza umuhimu wa kuwashirikisha wazazi kupitia mikutano na semina za uelimishaji.
“Mafanikio ya mradi huu hayatapimwa kwa idadi ya vitabu vilivyosambazwa au walimu waliopatiwa mafunzo, bali kwa mabadiliko ya kitabia kwa vijana, ongezeko la mahudhurio, kupungua kwa mimba za utotoni na kuimarika kwa ufaulu,” alisema Dkt. Kirei.
Kwa upande wao walimu walioshiriki katika uzinduzi huo wameishukuru serikali kwa kutoka Ithibati ya kitabu hicho kwani kimekuwa nguzo muhimu katika kubadilisha maisha ya wanafunzi katika kujitambua.












.jpeg)





.jpeg)






.jpeg)





.jpeg)


.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)














