Na Janeth Raphael MichuziTv - Bungeni Dodoma 

Rais wa Kenya, William Ruto, ametoa wito mzito kwa nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki kuharakisha mageuzi ya sera yatakayorahisisha usafiri wa watu, bidhaa na huduma ndani ya ukanda huo. 

Akilihutubia Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania leo Jumanne Mei 5, 2026 jijini Dodoma,Rais Ruto alisisitiza kuwa maendeleo ya kweli ya kiuchumi hayawezi kupatikana bila kuondoa vikwazo visivyo vya lazima vinavyokwamisha shughuli za wananchi mipakani.

Katika hotuba yake, Rais Ruto alieleza kuwa uhalisia wa maisha ya wananchi wa Afrika Mashariki tayari umevuka mipaka ya kisiasa, ambapo watu wanaishi, kufanya kazi na kuendesha biashara katika nchi tofauti ndani ya ukanda huo. Alibainisha kuwa ni wajibu wa serikali kuhakikisha sera na mifumo ya kiuchumi inaendana na hali hiyo ili kurahisisha maisha ya wananchi na kukuza uchumi wa pamoja.

Alisisitiza kuwa wafanyabiashara wadogo na wa kati ndio uti wa mgongo wa uchumi wa Afrika Mashariki, lakini bado wanakumbana na changamoto nyingi zikiwemo urasimu wa mipakani, tozo zisizo rafiki na taratibu ngumu za usafirishaji. Kwa mujibu wake, kuboresha mazingira ya biashara kwa kundi hili kutakuwa kichocheo kikubwa cha ukuaji wa uchumi wa kikanda na kuongeza ajira kwa vijana.

Rais Ruto pia aligusia mshikamano wa kijamii na kihistoria uliopo kati ya mataifa ya Afrika Mashariki, akieleza kuwa familia nyingi zinaishi pande zote za mipaka, jambo linalodhihirisha kuwa umoja wa wananchi tayari upo kwa vitendo. Aliongeza kuwa kinachohitajika sasa ni sera na mifumo ya kiserikali inayounga mkono uhusiano huo na kuondoa vikwazo vinavyowagawa wananchi.

Kwa mfano wa kuvutia, alirejea uhamaji wa wanyamapori kati ya Serengeti National Park na Maasai Mara, akisema kuwa hata asili inaonesha wazi kuwa mipaka haipaswi kuwa kikwazo cha mshikamano. Alisisitiza kuwa kama wanyamapori wanaweza kuhamia kwa uhuru, basi binadamu nao wanapaswa kuwezeshwa kufanya hivyo kwa manufaa ya pamoja.

Aidha, Rais Ruto alizitaka nchi wanachama wa East African Community (EAC) kujifunza kutokana na makosa ya nyuma yaliyopelekea kusambaratika kwa jumuiya hiyo mwaka 1977. Alisisitiza kuwa mafanikio ya sasa yanapaswa kulindwa kwa dhamira ya kweli ya kisiasa, uwazi na ushirikiano wa karibu kati ya nchi wanachama.

Hotuba hiyo imekuja wakati ambapo juhudi za kuimarisha ushirikiano wa kikanda zinaendelea kushika kasi, huku viongozi wakitambua umuhimu wa soko la pamoja, uhuru wa usafiri na biashara huria. Kauli ya Rais Ruto imeweka msisitizo mpya katika ajenda ya kuondoa vikwazo vya kikanda, ikiwa ni sehemu ya mkakati mpana wa kujenga Afrika Mashariki yenye ushindani wa kiuchumi na fursa sawa kwa wananchi wake.

Kwa ujumla, ujumbe wa Rais Ruto unaashiria hitaji la dharura la mageuzi ya kisera yatakayowezesha Afrika Mashariki kufikia ndoto yake ya kuwa eneo lenye mshikamano, maendeleo na ustawi wa pamoja kwa vizazi vya sasa na vijavyo.



Mkoa wa Dodoma ni miongoni mwa Mikoa 21 ya Tanzania Bara inayotarajiwa kufanya utekelezaji wa Mradi wa Scale wenye lengo la kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabia nchi yanayoendelea kudhihirika kila wakati na kuwa tishio kwa uzalishaji wa chakula na ustawi wa mazingira.

Hayo yamesemwa na Katibu Tawala Msaidizi Sehemu ya Uchumi na Uzalishaji Bi. Aziza Mumba alipokua akifungua mafunzo ya siku mbili ya kuwajengea uwezo waratibu wa Halmashauri, Mkoa na timu zinazosimamia utekelezaji wa Mradi wa Scale yanayofanyika kwenye ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Jengo la Mkapa Jijini hapa Mei 04, 2026.

“Programu ya Scale ina lengo la kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabia nchi ambayo yapo bayana kutokana na baadhi ya maeneo kupata mvua chini ya wastani, mfano eneo lilikuwa likipata mvua kwa siku 70 lakini limepata kwa siku 35 au chini ya hapo, pia kiasi cha mvua ni nusu ya ambacho huwa inanyesha kila mwaka, hivyo kina athiri uzalishaji ambapo tulizalisha kwa 49% chini ya lengo tulilokuwa tumepanga”.

Katika wasilisho lake juu ya utekelezaji wa Mradi huo, Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Kati Hombolo Dr. Rogers Rugeiyamu amesema lengo kuu la Mradi ni kuimarisha Mifumo ya Serikali Kuu na Serikali za mitaa ili kuongeza ustahimilivu dhidi ya mabadiliko ya tabia nchi na kuwezesha uwekezaji kwa miradi inayoibuliwa na wanajamii wenyewe katika maeneo yaliyo hatarini.

Ameongeza kuwa, Mradi huo ni wa miaka mitano kuanzia 2025/26 hadi 2030 ukihusisha Halmashauri 65 kwa Tanzania Bara na Zanzibar ambapo kwa Bara ni Halmashauri 54 na Zanzibar 11, ukitekelezwa kwa fedha za Ruzuku kwa 90% huku mchakato wa matumizi ya ukiwa shirikishi, ambapo bajeti kuu ni Dola Milioni 110 zitakazotolewa na Benki ya Dunia,  10% zitakua Ruzuku na 90% italenga matumizi ya Halmashauri.
















-Agawa vifaa vya michezo kwa timu zote zinazoshiriki Ligi ya wilaya ya Mkinga


Na Oscar Assenga, MKINGA

Mbunge wa Jimbo la Mkinga mkoani Tanga (CCM), Twaha Mwakioja, ameahidi kushirikiana na wadau mbalimbali wa michezo kuinua kiwango cha soka wilayani humo kwa kuwekeza katika elimu na maendeleo ya waamuzi pamoja na makocha.

Akizungumza wakati wa mchezo wa Ngao ya Jamii uliokwenda sambamba na uzinduzi wa Ligi ya Wilaya ya Mkinga, uliofanyika katika Uwanja wa Chamazi, Kata ya Matamba, Mwakioja alisema lengo lao ni kuwekeza katika michezo kwa vijana ili kuwapatia ajira, kuboresha afya zao, pamoja na kuimarisha amani, mahusiano mema na ushirikiano miongoni mwao.

Alieleza kuwa dhamira yao ni kuwashika mkono vijana ili waweze kupiga hatua kutoka ngazi ya wilaya, kwenda mkoa, kanda na hatimaye ligi za juu, huku yeye akiwa bega kwa bega nao kuhakikisha wanafikia malengo yao.

Mbunge huyo alibainisha kuwa wamepata taarifa ya kuwepo kwa changamoto mbalimbali, ikiwemo uhaba wa makocha na waamuzi wenye sifa. Hivyo, wamejipanga kuwekeza katika mafunzo ya makocha ili kila kata iwe na angalau kocha mmoja mwenye ujuzi na mafunzo rasmi, pamoja na kuandaa waamuzi wenye vyeti ili kuboresha usimamizi wa michezo.

Alisisitiza kuwa uwekezaji huo utaenda sambamba na ushirikiano na Chama cha Soka Wilaya ya Mkinga katika kukuza na kuendeleza vipaji vya vijana.

Aidha, alisema mpango wao ni kuhakikisha kila kata na kijiji kinakuwa na timu ya mpira wa miguu inayoshiriki ligi ya wilaya. Aliongeza kuwa watawekeza zaidi ili kuibua timu imara zitakazoweza kushiriki ligi za ngazi ya mkoa, kanda na hatimaye Ligi Kuu, hatua itakayosaidia kuitangaza Mkinga katika ramani ya soka nchini.

Katika kuonyesha dhamira hiyo, Mwakioja alikabidhi jezi na mipira kwa timu zinazoshiriki ligi hiyo, ikiwa ni sehemu ya kuhamasisha na kusaidia maendeleo ya michezo wilayani humo.

Kwa upande wake, Katibu wa Chama cha Soka Wilaya ya Mkinga, Fadhili Habibu, alisema ratiba ya ligi hiyo imeanza Mei 4 katika kituo cha Mkinga, huku kituo cha Maramba kikitarajiwa kuanza Mei 6 (Jumatano), ambapo kutakuwa na vituo vinne vitakavyochezwa katika Kijiji cha Maramba, ikiwa ni pamoja na mechi kati ya Viva Dynamo na Maramba FC.

Habibu alisema lengo la ligi hiyo ni kusimamia na kuibua vipaji vya vijana, pamoja na kuwapa mwelekeo wa maendeleo yao kisoka. Alimshukuru mbunge kwa kujitoa na kushirikiana nao katika kufanikisha malengo hayo.

Naye Mwenyekiti wa Chama cha Soka Wilaya ya Mkinga, Hassan Zumo, alimpongeza mbunge kwa juhudi zake za kuendeleza michezo wilayani humo, akieleza kuwa hatua hiyo imeongeza hamasa na matarajio ya ushindani mkubwa katika ligi hiyo, hasa baada ya timu kukabidhiwa vifaa.

Zumo aliongeza kuwa tangu kuanzishwa kwa chama hicho mwaka 2008, wamekuwa wakipeleka vilabu katika mashindano ya ngazi ya mkoa lakini wamekuwa wakikwama kutokana na changamoto za kifedha. Hata hivyo, alisema kupitia uongozi wa Mbunge Mwakioja, wana matumaini ya kupata timu itakayoweza kufika hadi Ligi Kuu.

Aidha, timu zinazoshiriki mashindano hayo zimeahidi kujituma na kupambana kwa juhudi zote ili kuhakikisha ligi hiyo inaleta mafanikio na tija kwa vijana wa Wilaya ya Mkinga.

Mwisho.




















SHIRIKA la Uwakala wa Meli Tanzania na Mamlaka ya Udhibiti wa usafiri wa Majini nchini Kenya wamesaini mkataba wa utambuzi wa vyeti vya mabaharia na hati ya makubaliano kuhusu ushirikiano na usimamizi wa sekta ya usafiri wa njia ya maji baina ya nchi hizo mbili.

Mkataba huo umesainiwa na Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC) Mohamed Salum na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa usafiri wa Majini nchini Kenya CPA Omaye Nyarandi mbele ya Marais, Samia Suluhu Hassan na Rais William Ruto katika Hafla iliyofanyika Mei 4, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam
Na Karama Kenyunko Michuzi Tv

RAIS wa Kenya William Ruto amesema ushirikiano wa kibiashara kati ya Tanzania na Kenya utakuwa chachu ya kukuza uchumi na kupanua fursa za ajira kwa wananchi wa mataifa hayo mawili, hususan vijana.

Ruto ametoa kauli hiyo akisisitiza umuhimu wa uwekezaji wa pamoja katika miradi ya kimkakati, ikiwemo mpango wa kujenga kiwanda cha kusafisha mafuta mkoani Tanga.

Amesema serikali ya Kenya, pamoja na nchi nyingine ikiwemo Uganda, iko tayari kushiriki katika utekelezaji wa mradi huo, ambao utafungua milango ya biashara na kukuza viwanda katika ukanda huo.

“Watu wa Tanzania, nyinyi ni wenye bahati kwamba tunajadili namna ya kujenga kiwanda cha kusafisha mafuta huko Tanga. Serikali ya Kenya iko tayari kufanya hilo, na pia Uganda iko tayari. Hii ni fursa ya pamoja ya kujenga mfumo wa amani wa biashara na viwanda hapa hapa Tanga,” amesema Ruto.

Aidha, ameeleza kuwa ukaribu wa kijiografia kati ya Tanga na Mombasa, ambao ni takribani kilomita 190, pamoja na uwepo wa miundombinu ya bomba la mafuta kutoka Mombasa, utarahisisha utekelezaji wa mradi huo na kuimarisha biashara ya kikanda.

Mbali na sekta ya mafuta, Rais Ruto ameibainisha kuwa kuna fursa pia katika uchakataji wa madini, akisisitiza kuwa wakati umefika kwa nchi za Afrika Mashariki kuacha kuuza malighafi nje bila kuongeza thamani.

“Tunapaswa kuacha kuuza nje malighafi. Kwa kufanya hivyo tunauza nje ajira, fursa na utajiri wetu. Badala yake, tunahitaji kuchakata rasilimali zetu hapa hapa ili kuongeza thamani na kujenga uchumi imara na endelevu,” amesisitiza.

Ameongeza kuwa mazungumzo yake na Rais wa Tanzania yamelenga kuhakikisha kuwa rasilimali zilizopo zinatumika ipasavyo kwa manufaa ya wananchi wa eneo hili, akibainisha kuwa huo ndio mwelekeo sahihi wa maendeleo ya kiuchumi kwa sasa.

Kauli ya Ruto inaakisi dhamira ya nchi za Afrika Mashariki kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi na kupunguza utegemezi wa kuuza malighafi, hatua inayotarajiwa kuongeza ajira, kukuza viwanda na kuimarisha uchumi wa kikanda.


NA Nasra Ismail, Geita

Mkuu wa Mkoa wa Geita, Martin Shigela, amewataka wananchi kuacha tabia ya kupiga simu za majaribio au mzaha kwenye namba za dharura za Jeshi la Zimamoto na Uokoaji.

Akizungumza katika kilele cha Siku ya Zimamoto Duniani kilichofanyika kimkoa katika Kata ya Ludete, Katoro, Shigela amesema vitendo hivyo vinaleta usumbufu mkubwa na vinafanya jeshi kushindwa kuamini taarifa za dharura za kweli.

Kufuatia hali hiyo, amewaagiza viongozi wa kata na watendaji kuendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa kuheshimu majukumu ya vyombo vya ulinzi na usalama, hususani Zimamoto, ambacho kinatoa huduma ya moja kwa moja ya kuokoa maisha na mali zao.

Hadi kufikia Mei jumla ya matukio 82 yamepatikana mkoani Geita ambapo matukio ya moto yalikuwa 32, matukio ya maokozi 50 huku jumla matukio yaliyosababisha majeruhi ni 39 na vifo 32.

Kaimu kamanda wa zimamoto mkoa wa Geita Kennedy Mwakasitu ametoa wito kwa jamii kuendelea kutoa ushirikiano kwa jeshi Hilo ili liweze kufanya kazi zake kwa ufasaha.

Maadhimisho ya siku ya wazimoto duniani hufanyika Mei 4 ya Kila mwaka ambapo katika mkoa wa Geita yalifanyika katika Mamlaka ya mji mdogo wa Katoro yakiongozwa na matembezi pamoja na elimu juu ya matumizi ya nishati ya kupikia.

Wananchi waliopata Elimu hiyo wameishukuru jeshi la zimamoto kwa namna walivyojufunza namna ya kudhibiti gesi iliyovuja na kuripuka kwa urahisi ambapo hapo awali walikuwa wanapata mshtuko mkubwa unaopelekea maafa makubwa.




 


Hati ya makubaliano ya mashirikiano ya kuwajengea uwezo watumishi wa umma wa  Tanzania na Kenya  imesainiwa kati ya Dkt. Ernest Francis Mabonesho, Mtendaji Mkuu na Mkuu wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania, na Prof. Nura Mohamed, Mkurugenzi Mkuu wa Shule ya Serikali Kenya (Kenya School of Government), mbele ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, na Rais wa Kenya, Mhe. Dkt. William Samoei Ruto.

Hafla hiyo imefanyika  Ikulu, Jijini Dar es Salaam, leo tarehe 4 Mei 2026.
Makubaliano haya yanatarajiwa kuleta maendeleo makubwa katika sekta ya utumishi wa umma kwa kuimarisha mafunzo na ufanisi wa watumishi wa umma pamoja na kupanua ushirikiano wa kiutendaji kati ya nchi mbili.

KOCHA BINGWA WA MICHEZO YA UOGELEAJI AUSTIN PILLADO ATUA DAR, KUWEKA KAMBI SIKU 10


Na Mwandishi Wetu 


Na Mwandishi Wetu, Dar es salaamHATIMAYE Kocha maarufu kutoka Marekani, Austin Pillado ambaye pia ni Naibu Kocha Mkuu wa timu ya kuogelea kutoka Chuo Washington State, ametua nchini jana Jumapili kwa ajili ya kuendesha kambi maalumu ya mafunzo ya kuogelea kwa muda wa siku 10.

Kambi hiyo inayofanyika jijini Dar es Salaam, imeandaliwa na Shule ya Kimataifa ya Monti kwa kushirikiana na Chama cha Mchezo wa Kuogelea Nchini (TSA).

Akizungumza na waandishi wa habari katika mapokezi ya kocha huyo kwenye uwanja wa Uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi mkuu na Mwanzilishi wa shule hiyo ya Monti International, Fatma Fernandes alisema lengo kuu ni kuinua viwango vya vipaji vya ndani kufikia hadhi ya kimataifa.

“Hii ni siku ambayo tunaanza hatua muhimu ya kuinua michezo ya kuogelea na maendeleo ya vijana hapa nchini Tanzania.

“Kwa sababu mpango huu wa mafunzo ya kambi maalumu ya kuogelea unaendana kikamilifu na maono ya uongozi wetu wa kitaifa  kutoka kwa Rais Samia Suluhu Hassan katika kukuza vipaji vya vijana, hadi kwa Waziri Habari, Sanaa na Michezo, Paul Makonda katika kuhakikisha michezo yote inapewa nafasi ya kukua. 

“Sisi Monti International tunaamini kuogelea kunaweza kuwa nguzo muhimu ya michezo Tanzania, na sekta binafsi ina nafasi kubwa ya kuchangia katika kujenga mafanikio hayo,” amesema Fatma.

Naye Mwenyekiti wa TSA, David Mwasogye amesema ujio wa kocha huyo kutasaidia kupunguza au kuziba pengo kati ya vipaji vya ndani na viwango vya kimataifa. 

“Kwa kuwaleta makocha wa kiwango cha juu kama Austin, tunawezesha vijana wetu kupata mafunzo na uchambuzi wa kitaalamu sawa na wanariadha bora duniani,” alisema Mwasogye.

Aidha, Kocha Austin Pillado mbali na kupongeza utayari wa Watanzania kujifunza na kupokea changamoto mpya, alisema Tanzania ina vipaji vingi lakini vinahitaji kupewa fursa ya kupata mafunzo ya kiwango cha juu cha kushindana kimataifa.

“Ndiyo maana nimekuja hapa Tanzania kubadilishana uzoefu kutoka kwenye mfumo wa kimataifa wa NCAA, lengo ni kuona watoto na wakufunzi wanapata mafunzo yenye viwango sawa na wanamichezo bora duniani.

Kocha maarufu kutoka Marekani, Austin Pillado ambaye pia ni Naibu Kocha Mkuu wa timu ya kuogelea kutoka Chuo Washington State (katikati) akiwa ameshika bendera ya Tanzania sambamba na Mkurugenzi mkuu na Mwanzilishi wa shule hiyo ya Monti International, Fatma Fernandes (kushoto) na Mwenyekiti wa Chama cha Kuogelea Tanzania (TSA), David Mwasogye (kulia). Austin amekuja nchini kuongoza kambi ya siku 10 ya mafunzo maalumu ya kuogelea jijini Dar es Salaam.

Kocha maarufu kutoka Marekani, Austin Pillado ambaye pia ni Naibu Kocha Mkuu wa timu ya kuogelea kutoka Chuo Washington State na Mkurugenzi mkuu na Mwanzilishi wa shule ya Monti International, Fatma Fernandes (kushoto) wakicheza pamoja na wasanii katika mapokezi yake jijini Dar es salaam. Austin amekuja nchini kuongoza kambi ya siku 10 ya mafunzo maalumu ya kuogelea jijini Dar es Salaam. 


Na Karama Kenyunko,Michuzi TV.

SERIKALI ya Tanzania na Kenya zimesaini mikataba nane ya makubaliano yenye lengo la kuimarisha sekta mbalimbali za maendeleo katika nchi hizo mbili

Hafla ya utiaji saini mikataba hiyo imefanyika leo Mei 4, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam baina ya mawaziri na watendaji wa sekta husika, ikishuhudiwa na Rais Dkt.Samia Suluhu Hasaan na Rais wa Kenya William Ruto ambaye yupo nchini kwa ziara ya kikazi ya siku mbili.

Mkataba wa kwanza uliosainiwa ni hati ya makubaliano kuhusu ushirikiano wa uendelezaji na usimamizi wa reli kati ya serikali ya Tanzania na Kenya, na wa pili unahusu upembuzi yakinifu kwa ajili ya mradi wa ujenzi wa bomba la gesi asilia kutoka Dar es Salaam hadi Mombasa.

Mkataba wa tatu ni kuhusu usaidizi wa kisheria katika masuala ya jinai kati ya serikali hizo mbili na wa nne ni makubaliano kuhusu masuala ya kilimo kati ya Tanzania na Kenya huku wa tano ukihusu utambuzi wa vyeti vya mabaharia.

Mkataba wa sita ni hati ya makubaliano wa kuimarisha uhusiano na usimamizi wa sekta ya usafiri wa njia ya maji , mkataba wa saba ni ushirikiano kati ya taasisi ya viwango Zanzibar na shirika la viwango la Kenya.

Pia wa nane ukiwa ni hati ya makubaliano kati ya vyuo vya utumishi wa umma vya Tanzania na Kenya kuhusu kujengeana uwezo katika masuala ya utumishi wa umma ambapo mikataba hiyo minane ilielezwa kuwa ishara ya ushirikiano unaozidi kuimarika kati ya Tanzania na Kenya.

Kuhuzu ziara ya kiongozi huyo, Rais Dkt.Samia amesema kuwa ziara ya Rais Ruto imekuwa ya kiserikali na imelenga kuimarisha uhusiano kati ya Tanzania na Kenya pamoja na kujadili maendeleo na uwekezaji.

“Rais wa Kenya mara nyingi amekuwa akija Tanzania kwa shughuli mbalimbali, lakini leo amekuja kwa ziara rasmi ya kiserikali.

“Katika ziara hii tumefanya mazungumzo muda mfupi uliopita kuangalia maendeleo ya nchi zetu lakini pia tumezungumza masuala ya siasa na ulinzi na kukuza uwekezaji katika nchi zetu,” amesema Rais Dk.Samia.

Aidha, Rais Samia ameeleza kuwa wamekubaliana katika miradi ya maendeleo ikiwemo bomba la gesi pamoja na sekta ya uchukuzi na miundombinu.“Tumekubaliana pia kuhusu bomba la gesi kutoka Tanzania Dar es Salaam kuelekea Mombasa Kenya na kama mlivyoshuhudia tumesaini maelewano.

“Pia kwenye uchukuzi na miundombinu tumekubaliana kwenye reli kutoka Bandari ya Tanga itapita Kilimanjaro hadi Kenya na usafiri wa ndani ya maji katika maziwa yetu hasa Ziwa Victoria kuunganisha biashara ya Kenya na Tanzania,” amesema.







Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Kenya Mhe. Dkt. William Samoei Ruto wakishuhudia utiaji saini wa Mikataba 8 ya Ushirikiano baina ya Tanzania na Kenya katika sekta mbalimbali kabla ya kuzungumza na Waandishi wa Habari, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 04 Mei, 2026. Mikataba 8 iliyosainiwa ni kuhusu masuala ya usimamizi wa Reli, upembuzi yakinifu wa mradi wa bomba la Gesi kutoka Dar es Salaam hadi Mombasa, usaidizi wa Kisheria kuhusu masuala ya jinai, masuala ya Kilimo, utambuzi wa vyeti vya Mabaharia, usimamizi wa sekta ya Usafiri kwa njia ya maji, masuala ya Viwango pamoja na kujengeana uwezo kwenye masuala ya Utumishi wa Umma.

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.
Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na Rais wa Jamhuri ya Kenya
Mhe. Dkt. William Samoei Ruto mara baada ya kuwasili katika viwanja
vya Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa Ziara ya Kitaifa tarehe 04 Mei, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Kenya Mhe. Dkt. William Samoei Ruto mara baada ya kuwasili katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa Ziara ya Kitaifa tarehe 04 Mei, 2026.

. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa amesimama na Rais wa Jamhuri ya Kenya Mhe. Dkt. William Samoei Ruto wakati wimbo wa Taifa ukiimbwa katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 04 Mei, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Kenya Mhe. Dkt. William Samoei Ruto akikagua Gwaride lililoandaliwa kwa heshima yake na Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 04 Mei, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Kenya Mhe. Dkt. William Samoei Ruto akisalimiana na viongozi mbalimbali waliofika kumpokea katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 04 Mei, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Kenya Mhe. Dkt. William Samoei Ruto wakati wakielekea katika ukumbi wa Kikwete kwa ajili ya mazungumzo, tarehe 04 Mei, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Kenya Mhe. Dkt. William Samoei Ruto akisaini Kitabu cha Wageni mara baada ya kuwasili katika ukumbi wa Kikwete, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 04 Mei, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Kenya Mhe. Dkt. William Samoei Ruto akisaini Kitabu cha Wageni mara baada ya kuwasili katika ukumbi wa Kikwete, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 04 Mei, 2026.



Top News