Na Immaculate Makilika - MAELEZO

Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Paul Makonda amewataka wadau wa sekta ya habari kubadili ajenda ya kutangaza watu badala yake watangaze fursa za uchumi zilizopo nchini.

Ametoa rai hiyo leo Aprili 30, 2026 katika Siku ya Tatu ya Maadhimisho ya Siku ya Uhuru wa Vyombo vya Habari Duniani iliyofanyika jijini Arusha.

“ Tuache ajenda ya kutangaza watu, tuitangaze nchi yetu. Tubadilishe mkakati kutoka ajenda ya kusifia watu, tuambieni fursa za uchumi zilizopo,” amesema Waziri Makonda

Ameongeza kuwa waandishi wa habari waache kasumba ya kuwaandika vizuri wala rushwa na watu wasio na sifa njema katika jamii, badala yake wafanye kazi zao kwa maslahi ya Taifa.

Ametolea mfano kuwa hakuna idadi ya kutosha ya waandishi wanaoandika kuhusu sekta ya utalii au kilimo kama wanaoandika kuhusu masula ya siasa.

Amezungumzia kuhusu Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 na kuwaasa waandishi wa habari kushiriki kikamilifu ili kufikia malengo yaliyowekwa huku akisisitiza kuhusu umuhimu wa mchango wa Vvyombo vya Habari kwa maendeleo ya nchi.

Aidha, Waziri Makonda amewataka waandishi wa habari kujiridhisha na vyanzo vya taarifa za kabla ya kuzisambaza kwa umma ili kuepuka upotoshaji na migogoro.

Kuhusu mapendekezo yaliyotelewa na wadau wa sekta ya habari ya kuboresha utendaji wa sekta hiyo nchini, Mhe. Makonda amesema Serikali imeyapokea mapendekezo yote 15 na itayafanyia kazi kwa kushirikiana na wadau.

Naye, Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Bw. Gerson Msigwa amesema kuwa lengo la Maadhimisho ya Siku ya Uhuru wa Vyombo vya Habari Duniani ni kutathimi na kulinda hali ya uhuru wa Vyombo vya Habari Duniani.

Ameongeza kuwa kupitia Maadhimisho hayo Serikali itapata fursa ya kukutana na washirika wake wa maendeleo na asasi za kiraia kujadili masuala ya mabadiliko ya utendaji kazi katika sekta ya habari pamoja na kuwaendeleza watayarishaji wa maudhui.

Naye, Mkurugenzi wa Taasisi ya Tech and Media Convergency (TMC) na Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya Maadhimisho hayo kwa mwaka 2026, Bi. Asha Abinallah amesema kuwa kupitia Maadhimisho hayo wadau wameandaa mapendekezo kadhaa ikiwemo kuitaka Serikali kuharakisha uanzishwaji wa Mfuko wa Habari na kuandaa sera rafiki za kuvutia uwekezaji katika sekta ya habari.

Vilevile, wameitaka Serikali kupitia Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) kuendelea kutimiza majukumu yake ikiwemo kuwajengea uwezo wanahabari katika matumizi ya akili unde.










MAHAKAMA Kuu Masijala Ndogo Dar es salaam, imetupilia mbali maombi ya Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Tundu Lissu ya kuomba kuunganishwa katika kesi ya mgawanyo wa mali iliyofunguliwa na Makamu Mwenyekiti wa chama hicho Zanzibar, Said Issa Mohamed, pamoja na wenzake.

Wengine waliofungua kesi hiyo hiyo ni wajumbe wa bodi ya wadhamini wa Zanzibar Ahmed Rashid Khamis na Maulidah Anna Komu (marehemu).

Wajibu maombi katika kesi hiyo namba 8323 ya mwaka 2025  ambao ni Bodi ya Wadhamini ya Chadema upande wa bara na Katibu Mkuu wa chama hicho, John Mnyika.

Uamuzi huo mdogo umetolewa na Jaji Hamidu mwanga ambaye awali alikuwa akikisikikiza shauri hilo na umesomwa leo Aprili 30, 2026  na Naibu Msajili ya Mahakama hiyo, Hussein Mushi.

Awali, kesi hiyo ilikuwa ikisikilizwa mbele ya Jaji Mwanga kama ilivyoelezwa, huku Lissu aliomba kuunganishwa katika kesi hiyo akidai kuwa kwakuwa kesi hiyo inahusu chama na yeye ndiye mwenyekiti wa chama basi anapaswa kuwa sehemu ya kesi hiyo.

Maombi hayo yalisikilizwa na uamuzi ulipaswa kutolewa Machi 25, mwaka huu lakini kutokana na faili kuitwa Mahakama ya Rufaa Dodoma kesi hiyo ilipelekwa mbele hadi leo.

Katika uamuzi huo Mahakama imekataa kumuunganisha Lissu katika kesi hiyo kama mwenyekiti wa Chama lakini kwakuwa ameyapeleka kwa matakwa yake na si kwa nafasi yake hivyo hana maslahi ya moja kwa moja kwani cheo hicho kinaweza kukaliwa na mtu yeyote

Mahakama imeeleza kuwa Lissu anaweza kutokea kwenye kesi hiyo kama shahidi wakati wa usikilizwaji wa kesi ya msingi na si kama moja ya wajibu maombi

Akizungumza nje ya Mahakama Wakili wa chadema , Dkt. Rugemeleza Nshala amedai kesi hiyo kwa sasa imehamishiwa kwa Jaji David Ngunyale na inatarajiwa kutajwa Mei 13,2026.

"Kurudi kwa kesi hii kunaenda sambamba na kufuata maagizo ya mahakama ya Rufaa ya kumtaka Jaji huyo kuangalia kama maombi hayo yalipelekwa ndani ya muda au laa.

“Madai yanatakiwa yaletwe ndani ya miaka sita tangu kuanza kwa migogoro katika uamuzi wa leo wa Jaji Mwanga wakili wa upande wa walalamikaji alisema kwa msisitizo kwamba mgogoro ulianza mwaka 2016, hivyo jaji Ngunyale atatusaidia kuangalia ni muda gani kati ya 2016 hadi 2025,” ameeleza Dkt. Nshala.

Akizungumzia kesi ya uhaini dhidi ya Lissu,  Dkt Nshala bado hawajajua itapangwa lini kwa sababu kesi hiyo ipo katika Mahakama ya rufaa ambayo ndo inatarajiwa ipange mara nyingi hupangwa kwa muundo wa vikao, hivyo msajili wa Mahakama ya rufaa ndiyo atajua ipangwe lini,” amedai Dkt Nshala.





Na. Mwandishi Wetu, Morogoro

Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi imetoa wito kwa watendaji wa uchaguzi kuhakikisha wanatumia muda wao kusoma Katiba, sheria za uchaguzi, kanuni na maelekezo ya Tume ili waweze kusimamia uchaguzi kwa weledi.

Wito huo umetolewa na Makamu Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Mahakama ya Rufaa (Mst) Mbarouk Salim Mbarouk Mkoani Morogoro leo tarehe 30 Aprili, 2026 wakati akifunga mafunzo ya watendaji wa uchaguzi yaliyofanyika kwa siku tatu kuanzia tarehe 28 Aprili, 2026.

Mafunzo hayo ni sehemu ya mchakato wa maandalizi ya uchaguzi mdogo wa ubunge kwenye Jimbo la Ismani Halmashauri ya Wilaya ya Iringa, Mkoani Iringa na Kata 12 za Tanzania Bara unaotarajiwa kufanyika tarehe 01 Juni, 2026.

“Natumia nafasi hii kuendelea kuwasisitiza kuhusu umuhimu wa kutenga sehemu ya muda wenu kusoma Katiba, sheria na maelekezo mbalimbali yanayotolewa na Tume ili yawaongoze katika kusimamia uchaguzi utakaokuwa huru na wa haki,” amesema Jaji Mbarouk.

Amewataka watendaji hao wa uchaguzi kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi na weledi ili kufanikisha uchaguzi huo mdogo ambao unafanyika kujaza nafasi wazi ya mbunge na madiwani.

“Jukumu lililopo mbele yetu ni kubwa na muhimu, linahitaji umakini na kujituma. Ni matazamio ya Tume kwamba, baada ya kupatiwa mafunzo haya, mtatekeleza majukumu yenu kwa ufanisi na weledi mkizingatia ratiba ya utekelezaji ili kufanikisha uchaguzi mdogo wa ubunge katika Jimbo la Ismani na Kata 12 za Tanzania Bara unaotarajiwa kufanyika tarehe 01 Juni, 2026,” amesema Jaji Mbarouk.

Amesisitiza kuwa ili ufanisi uwepo ni muhimu watendaji hao wazingatie sifa na uwezo wakati wa kuteua na kuajiri watendaji wa vituo vya kupigia kura kwa kuwa hao ndio watakaosimamia zoezi la kupiga kura na kuhesabu kura vituoni.

“Kuhusu ajira za watendaji wa vituo, tunayo imani kuwa mtateua na kuajiri watendaji wenye sifa na uwezo wa kufanya kazi hii muhimu kwa kuwa hao ndio watakaosimamia zoezi la kupiga kura na kuhesabu kura vituoni. Kazi ambayo inahitaji umahiri, umakini na weledi katika kuitekeleza.,” amesema Jaji Mbarouk.

Amewataka watendaji hao kuhakikisha kuwa mafunzo ya watendaji wa vituo yanafanyika kwa ufanisi na weledi katika tarehe zilizopangwa kwenye ratiba ya utekelezaji wa shughuli za uchaguzi.

Ameongeza kuwa mafunzo hayo yanalenga kuwajengea uwezo ili waweze kufahamu majukumu yao na kuyatekeleza ipasavyo wakati wa uchaguzi.

Mafunzo hayo yamewahusisha Waratibu wa Uchaguzi wa Mikoa, Wasimamizi wa Uchaguzi, Wasimamizi Wasaidizi wa Uchaguzi Ngazi ya Jimbo, Wasimamizi wa Uchaguzi Ngazi ya Kata, Maafisa Uchaguzi, Maafisa Ununuzi na Wahasibu.

Kata 12 za Tanzania Bara zitakazofanya uchaguzi wa Udiwani ni Mzimuni iliyopo Manispaa ya Kinondoni; Zongomera, Manispaa ya Kahama; Itilo, Halmashauri ya Mji wa Nzega; Ketare, Halmashauri ya Mji wa Tarime na Nyumbigwa, Halmashauri ya Mji wa Kasulu.

Nyingine ni kata ya Kala iliyoko Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi; Ziba, Halmashauri ya Wilaya Igunga; Kamsisi, Halmashauri ya Wilaya ya Mlele; Nyamugali, Halmashauri ya wilaya ya Buhigwe; Namasakata Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru; Bwongera, Halmashauri ya Wilaya ya Chato na Kibiti Halmashauri ya Wilaya ya Kibiti.
Makamu Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Mahakama ya Rufaa (Mst) Mbarouk Salim Mbarouk akizungumza wakjati akifunga mafunzo ya watendaji wa uchaguzi yaliyofanyika Mkoani Morogoro. Mafunzo hayo yamefungwa leo tarehe 30 Aprili, 2026 na yaliyofanyika kwa siku tatu kuanzia tarehe 28 Aprili, 2026. (Picha na INEC). 
Sehemu ya watendaji wa uchaguzi katika jimbo la Isimani Mkoani Iringa na Kata 12 za Tanzania bara wakisikiliza hotuba ya kufunga mafunzo ya siku tatu yaliyofanyika mkoani Morogoro kuanzia tarehe 28 hadi 30 Aprili, 2026. (Picha na INEC).





Na Janeth Raphael- MichuziTv -Dodoma 

Serikali imesema imepokea rasmi ushauri wa wabunge kuhusu kuanzishwa kwa mfumo wa bima ya afya kwa wakulima, hususan wale wanaojihusisha na zao la korosho, huku ikiweka wazi kuwa tayari imeanza mchakato wa kufanya tathmini ya kina ili kubaini namna bora ya kutekeleza mpango huo.

Akizungumza bungeni jijini Dodoma Aprili 29, 2026 wakati akijibu hoja zilizotolewa na wabunge katika mjadala wa bajeti ya Wizara ya Kilimo kwa mwaka wa fedha 2026/2027, Waziri wa Kilimo, Daniel Chongolo, amesisitiza kuwa Serikali inatambua umuhimu wa pendekezo hilo na inalipa uzito unaostahili kutokana na mchango mkubwa wa wakulima katika uchumi wa taifa.

Ameeleza kuwa hatua ya awali ni kufanya uchambuzi wa kina utakaosaidia kubaini muundo sahihi wa bima hiyo, ikiwemo gharama, walengwa, na namna ya kuisimamia ili iweze kuwa endelevu na yenye manufaa kwa wakulima.

“Hoja ya bima ya afya kwa wakulima wa korosho tumeipokea. Tunakwenda kufanya tathmini ya kina ili kujua namna bora ya kuitekeleza. Baada ya hapo, tutakaa na wadau mbalimbali kuona jinsi ya kuanzisha mpango huo kwa ufanisi,” alisema Chongolo.

Aidha, Waziri huyo amebainisha kuwa mpango huo hautalenga wakulima wa korosho pekee, bali Serikali inalenga kuupanua ili kuwahusisha wakulima wa mazao mengine ya kimkakati kama pamba, tumbaku na mazao mengine yanayolimwa kwa wingi nchini.

Chongolo amesema kuwa lengo kuu la mpango huo ni kuboresha ustawi wa wakulima kwa kuwapatia kinga ya kiafya, jambo litakalowasaidia kufanya kazi zao kwa ufanisi zaidi na hatimaye kuongeza tija katika sekta ya kilimo.

Hatua hiyo inatajwa kuwa sehemu ya jitihada za Serikali za kuimarisha sekta ya kilimo, ambayo ni mhimili muhimu wa uchumi wa nchi, pamoja na kuhakikisha kuwa wakulima wanapata huduma bora za kijamii zinazowawezesha kushiriki kikamilifu katika shughuli za uzalishaji.

Wadau wa sekta ya kilimo wamekuwa wakisisitiza umuhimu wa kuwepo kwa mifumo ya hifadhi ya jamii kwa wakulima, wakieleza kuwa changamoto za kiafya mara nyingi huathiri uzalishaji na kipato chao. Kupitia mpango huu unaopendekezwa, inatarajiwa kuwa wakulima watanufaika kwa kupata huduma za afya kwa gharama nafuu au kwa mfumo unaowawezesha kumudu kulipia huduma hizo kwa urahisi zaidi.





Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma

Serikali kupitia Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari imeweka wazi mkakati wake wa kuendeleza sekta ya TEHAMA kwa kuwasilisha bungeni makadirio ya mapato na matumizi kwa mwaka wa fedha 2026/2027. Bajeti hiyo inalenga kuimarisha miundombinu ya mawasiliano pamoja na kukuza uchumi wa kidijitali nchini.

Akiwasilisha taarifa hiyo, Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Angellah Kairuki, amesema wizara inatarajia kukusanya jumla ya Shilingi 160,369,240,000. Mapato hayo yanatarajiwa kutokana na uuzaji wa huduma za Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano, ambao umeendelea kupanuka na kuongeza matumizi ndani na nje ya mipaka ya nchi.

Amesema kuwa ongezeko la makusanyo linachochewa na kuimarika kwa matumizi ya huduma za mawasiliano, sambamba na juhudi za serikali kueneza miundombinu ya intaneti hadi maeneo zaidi ya vijijini na mijini. Hatua hiyo inalenga kuhakikisha wananchi wengi zaidi wanapata huduma bora na za uhakika.

Kwa upande wa matumizi, wizara imeomba kuidhinishiwa jumla ya Shilingi 222,589,451,000 kwa ajili ya kutekeleza majukumu yake katika mwaka ujao wa fedha. Kiasi hicho kinajumuisha matumizi ya kawaida na fedha za miradi ya maendeleo.

Kati ya fedha hizo, Shilingi 13,146,172,000 sawa na asilimia 5.9 ya bajeti yote zimetengwa kwa matumizi ya kawaida. Ndani ya fungu hilo, Shilingi 6,371,830,000 ni kwa ajili ya mishahara ya watumishi, huku Shilingi 6,774,342,000 zikielekezwa kwenye gharama nyingine za uendeshaji wa wizara.

Sehemu kubwa ya bajeti hiyo, ambayo ni Shilingi 209,443,279,000 sawa na asilimia 94.1, imeelekezwa katika miradi ya maendeleo. Mgawanyo wa fedha hizo unaonesha kuwa Shilingi 98,480,905,000 ni fedha za ndani, wakati Shilingi 110,962,374,000 zitatoka kwa washirika wa maendeleo kutoka nje ya nchi.

Waziri Kairuki amesisisitiza kuwa uwekezaji huu mkubwa utaongeza upatikanaji wa huduma za mawasiliano, kuboresha kasi na ubora wa intaneti, pamoja na kufungua fursa mpya za kiuchumi kupitia teknolojia. Aidha, utawezesha sekta mbalimbali kama elimu, afya na biashara kunufaika zaidi na mapinduzi ya kidijitali.

Kwa ujumla, bajeti hiyo inalenga kuharakisha mageuzi ya kidijitali nchini, kuongeza ufanisi wa huduma za umma, na kuiweka Tanzania katika nafasi nzuri ya ushindani wa kiteknolojia ndani ya ukanda na kimataifa.


 

KATIBU Mkuu wa Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira Tanzania(TRAMEPRO) Boniventura Mwalongo amekutana na kufanya mazungumzo na Chifu Msangia Ongati Ngoje wa Rorya ambaye ni Makamu Mwenyekiti wa Machifu na Mzee wa Mila na Desturi Mkoa wa Mara.

Kikao hicho kilijikita katika kujadili mustakabali wa taifa letu, hususan katika maeneo ya utatuzi wa migogoro ya ardhi, maadili ya jamii, uadilifu katika utumishi wa umma, pamoja na dira ya maendeleo ya muda mrefu ya Tanzania.

Taarifa ya Makamu Mwenyekiti wa Machifu na Mzee wa Mila na Desturi Mkoa wa Mara Chifu Msangia Ongati Ngoje amesema katika kikao hicho, wamekubaliana kuimarisha nafasi ya mila na desturi katika utatuzi wa migogoro ya ardhi, kurejesha na kuendeleza maadili na uadilifu katika jamii na taasisi za umma.

Pia kujenga taifa lenye umoja, uwajibikaji na matumizi bora ya rasilimali. Aidha, walisisitiza umuhimu wa kuendeleza sekta ya tiba asili kama nyenzo ya afya na uchumi, na kulinda pamoja na kuendeleza utamaduni wa Waluo kama urithi muhimu wa taifa.

Amesena kama alivyosema mwanafalsafa mashuhuri William Shakespeare, “Ujinga ni laana; maarifa ni mabawa yanayotuinua juu.” ambapo nukuu hiyo inatukumbusha umuhimu wa sayansi, maarifa na elimu katika kuleta maendeleo endelevu ya jamii. 

Pia amesema, “Mguso mmoja wa asili huwafanya watu wote kuwa ndugu,” akisisitiza nafasi ya mazingira katika kuunganisha binadamu wote. 

Aidha, katika kuelezea maisha ya jamii na utamaduni wake, alisema, “Maisha yetu yamefumwa kwa nyuzi mchanganyiko—mema na mabaya pamoja,” jambo linalotukumbusha wajibu wa kuhifadhi mema ya utamaduni wetu na kurekebisha kasoro zilizopo.

Kwa upande wa uongozi wa kitaifa, amesema Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, amewahi kusisitiza kuwa, “Mila na desturi zetu ni utambulisho wetu kama taifa, ni wajibu wetu kuzilinda, kuziheshimu na kuzitumia kama chachu ya maendeleo endelevu.” 

Kauli hiyo inaonesha dhamira ya serikali katika kuendeleza urithi wa kitamaduni sambamba na maendeleo ya kisasa.

Kwa upande wa maendeleo ya eneo, Shirati ni Halmashauri ya Mji Mdogo iliyopo katika Wilaya ya Rorya, Mkoa wa Mara, Kaskazini mwa Tanzania, karibu na mpaka wa Kenya na kandokando ya Ziwa Victoria. 

“Mji huu unakadiriwa kuwa na wakazi kati ya 50,000 hadi 100,000, huku Wilaya ya Rorya ikiwa na takribani wakazi 354,490 kwa mujibu wa Sensa ya mwaka 2022. Idadi kubwa ya wakazi ni vijana wanaoishi vijijini.

“Shughuli kuu za kiuchumi katika eneo hili ni pamoja na kilimo kinachotegemewa na zaidi ya asilimia 80 ya wananchi, kikijumuisha mazao ya mahindi, mihogo, mtama, alizeti na pamba. 

“Uvuvi pia ni shughuli muhimu inayofanyika katika Ziwa Victoria ukihusisha samaki kama sangara, sato na dagaa. Aidha, wananchi hujihusisha na ufugaji wa ng’ombe, mbuzi na kondoo pamoja na biashara ndogo ndogo, ikiwemo biashara za mipakani kati ya Tanzania na Kenya.”

Amesema Kijiografia, eneo la Shirati liko katika Mkoa wa Mara, kaskazini mwa Tanzania, karibu na mpaka wa Kenya na kuzungukwa na Ziwa Victoria, likiwa na hali ya hewa ya kitropiki yenye mvua za msimu. Hali hii huchangia kwa kiasi kikubwa shughuli za kiuchumi na maisha ya wananchi wa eneo hilo.

Amesema utamaduni wa Waluo unaendelea kuwa nguzo muhimu ya mshikamano wa jamii, ukijengwa juu ya heshima kwa wazee na viongozi wa mila, matumizi ya baraza la wazee katika utatuzi wa migogoro, mshikamano wa kifamilia na kijamii, pamoja na kuzingatia maadili ya uadilifu, uwajibikaji na upendo. 

Pamoja na hayo amesema ni wazi  ushirikiano kati ya viongozi wa mila na desturi, serikali, wataalamu na wananchi ni muhimu katika kujenga jamii yenye maadili imara, uchumi thabiti na maendeleo endelevu. 

“Tunatoa mwito kwa wadau wote kushiriki kikamilifu katika kulinda mazingira, kuendeleza tiba asili, kuhifadhi utamaduni wa Waluo na kutumia vyema fursa zilizopo kwa maendeleo ya Mkoa wa Mara na taifa kwa ujumla,”amesema Chifu Msangia Ongati Ngoje wa Rorya. 

Mkuu wa Mkoa wa Singida, Bi. Halima Dendego, amepongeza mchango wa wadau mbalimbali ikiwemo Benki ya Taifa ya Biashara (NBC), katika kuunga mkono juhudi za Serikali za kuharakisha maendeleo ya sekta ya kilimo huku akiitaja kampeni ya “Wekeza NBC Shambani Ushinde” kuwa nyenzo muhimu ya kuimarisha ustawi wa wakulima na kuchochea ukuaji wa uchumi wa mkoa huo.

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa kampeni hiyo iliyofanyika jana Singida, Bi. Dendego alisema ujio wa mpango huo kwa mara ya kwanza mkoani humo ni hatua muhimu inayochochea utekelezaji wa malengo ya Serikali ya kuongeza uzalishaji wa mazao ya kimkakati na kuinua kipato cha wakulima.

Hafla hiyo iliwakutanisha wadau mbalimbali wa sekta ya kilimo, wakiwemo viongozi wa vyama vya msingi na vyama vikuu vya ushirika, wakulima, pamoja na washiriki wengine katika mnyororo wa thamani wa kilimo. Uongozi wa NBC katika uzinduzi huo uliwakilishwa na Mkuu wa Idara ya Bima, Bw. Benjamini Nkaka, pamoja na Mkuu wa Kitengo cha Wateja Wadogo na Wakulima, Bw. Raymond Urassa, wakiongoza timu ya maofisa wa benki hiyo akiwemo Mkuu wa Kanda ya Kati, Bw Miraji Msuya.

Kwa mujibu wa Bi. Dendego, ujio wa kampeni hiyo unaenda sambamba na jitihada za Serikali ambazo tayari zimeanza kuzaa matunda, ikiwemo usajili wa zaidi ya asilimia 92 ya wakulima mkoani Singida, utoaji wa ruzuku za pembejeo kama mbegu na mbolea, pamoja na uwekezaji katika huduma za ugani na kilimo cha umwagiliaji.

“Kampeni ya NBC Shambani inakuja kuimarisha juhudi hizi kwa kuchochea ujumuishaji wa kifedha kwa wakulima. Hii ni hatua muhimu kuelekea kilimo chenye tija na chenye manufaa kwa wananchi mmoja mmoja, kaya na mkoa kwa ujumla,” alisisitiza.

Aidha, RC Dendego aliwahimiza wakulima kuchangamkia fursa zinazotolewa na kampeni hiyo, akitaja baadhi ya manufaa yake kuwa ni pamoja na akaunti zisizo na makato ya kila mwezi, upatikanaji wa mikopo ya pembejeo na zana za kilimo, elimu ya fedha, pamoja na huduma za bima ya afya na mazao.

Akitoa ufafanuzi kuhusu kampeni hiyo, Bw. Nkaka alisema NBC inaendelea kubuni suluhisho bunifu za kifedha ili kuunga mkono azma ya Serikali ya kuongeza ukuaji wa sekta ya kilimo kutoka asilimia 5 hadi 10 ifikapo mwaka 2030. Alibainisha kuwa benki hiyo imejikita pia katika utoaji wa elimu ya fedha, huduma za kidijitali, pamoja na bima zinazolenga kupunguza hatari kwa wakulima.

Kwa upande wake, Bw. Urassa alisema kampeni hiyo ya miezo minne, inalenga wakulima wa mazao ya dengu, choroko, mbaazi, soya na ufuta, na inatoa fursa kwa wakulima binafsi pamoja na kupitia vyama vya ushirika kushiriki na kushinda zawadi mbalimbali, ikiwemo pikipiki na kompyuta mpakato (laptops).

“Lengo kuu ni kuwahamasisha wakulima kutumia mifumo rasmi ya kifedha kwa kutunza fedha zao benki. Tunawakaribisha kufungua akaunti za NBC Shambani ili waweze kunufaika na huduma na fursa hizi,” alieleza.

Baadhi ya wakulima walioshiriki uzinduzi huo walieleza matumaini yao juu ya kampeni hiyo, wakihimiza wenzao kuitumia vyema ili kunufaika na fursa za kifedha, elimu, bima na zawadi zinazotolewa.






Mkuu wa Mkoa wa Singida, Bi. Halima Dendego (wa tatu kulia), akionesha baadhi ya zawadi zinazotolewa kwa washindi kampeni ya “Wekeza NBC Shambani Ushinde” inayoratibiwa na Benki ya NBC, yenye lengo la kuhamasisha uzalishaji wa mazao ya kimkakati ikiwemo dengu, choroko, mbaazi, soya na ufuta mkoani humo. Hafla ya uzinduzi wa kampeni hiyo ilifanyika jana kwa kushirikisha wadau mbalimbali wa sekta ya kilimo, wakiwemo viongozi wa vyama vya ushirika pamoja na wakulima. Wengine pichani ni Mkuu wa Kanda ya Kati wa NBC, Bw Miraji Msuya (wa tatu kushoto), Mkuu wa Idara ya Bima wa NBC, Bw. Benjamini Nkaka (wa pili kushoto) Mkuu wa Kitengo cha Wateja Wadogo na Wakulima wa NBC, Bw. Raymond Urassa (kushoto), Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya Chama Kikuu cha Ushirika cha Wakulima wa Mkoa wa Singida (SIFACU) Bw Julius Kitundu (kulia) na Mrajisi Msaidizi wa Mkoa wa Singida Bi Nuria Gulamali (wa pili kulia)






Mkuu wa Mkoa wa Singida, Bi. Halima Dendego (katikati), akipokea zawadi maalum ya picha yake kutoka kwa wafanyakazi wa benki ya NBC wakiongozwa na Mkuu wa Kanda ya Kati wa NBC, Bw Miraji Msuya (kushoto) wakati wa hafla ya uzinduzi wa kampeni ya “Wekeza NBC Shambani Ushinde” inayoratibiwa na Benki ya NBC, yenye lengo la kuhamasisha uzalishaji wa mazao ya kimkakati ikiwemo dengu, choroko, mbaazi, soya na ufuta mkoani humo.






Akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa kampeni hiyo iliyofanyika jana Singida, Bi. Dendego (pichani) alisema ujio wa mpango huo kwa mara ya kwanza mkoani humo ni hatua muhimu inayochochea utekelezaji wa malengo ya Serikali ya kuongeza uzalishaji wa mazao ya kimkakati na kuinua kipato cha wakulima.






Akitoa ufafanuzi kuhusu kampeni hiyo, Bw. Nkaka (pichani) alisema NBC inaendelea kubuni suluhisho bunifu za kifedha ili kuunga mkono azma ya Serikali ya kuongeza ukuaji wa sekta ya kilimo kutoka asilimia 5 hadi 10 ifikapo mwaka 2030.






Kwa upande wake, Bw. Urassa (pichani) alisema kampeni hiyo ya miezo minne, inalenga wakulima wa mazao ya dengu, choroko, mbaazi, soya na ufuta, na inatoa fursa kwa wakulima binafsi pamoja na kupitia vyama vya ushirika kushiriki na kushinda zawadi mbalimbali, ikiwemo pikipiki na kompyuta mpakato (laptops).




Mrajisi Msaidizi wa Mkoa wa Singida Bi Nuria Gulamali akizungumza kwenye hafla hiyo.






Meneja wa Benki ya NBC tawi la Singida Bw David Mushi akizungumza kwenye hafla hiyo.






Baadhi ya maofisa wa NBC wakifafanua kuhusu huduma mablimbali za benki hiyo mahususi kwa wakulima.






Katika hafla hiyo wakulima walipata wasaa wa kusikiliza na kutoa mrejesho kuhusu huduma mbalimbali za benki hiyo.


Hafla hiyo iliwakutanisha wadau mbalimbali wa sekta ya kilimo, wakiwemo viongozi wa vyama vya msingi na vyama vikuu vya ushirika, wakulima, pamoja na washiriki wengine katika mnyororo wa thamani wa kilimo.

Kamishna wa Operesheni na Mafunzo wa Jeshi la Polisi (CP) Awadh Juma amefika Jijini Arusha kwa ajili ya kufanya ukaguzi wa miundombinu pamoja na mifumo ya kiusalama katika uwanja unaojengwa kwa ajili ya mashindano ya Mataifa ya Afrika (AFCON).

Katika ukaguzi huo, CP Awadh amepitia maeneo mbalimbali ya uwanja huo, ikiwemo mifumo ya usalama pamoja na eneo lililotengwa kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha Polisi ndani ya uwanja huo.

Amesema kuwa Jeshi la Polisi limejipanga kikamilifu kuhakikisha usalama unaimarishwa wakati wote, kabla na baada ya mashindano hayo muhimu kwa bara la Afrika.

Aidha, amesisitiza kuwa Watanzania wanapaswa kuendelea kudumisha sifa nzuri iliyojengwa na waasisi wa Tanzania waliohubiri amani na utulivu, huku akiwaomba wananchi kuwapokea vyema wageni watakaofika kutoka mataifa mbalimbali kushuhudia mashindano ya AFCON.

Katika ziara hiyo ya ukaguzi, CP Awadh aliambatana na Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani Mkoa wa Arusha, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Zauda Mohamed, pamoja na Mkuu wa Operesheni za Polisi Mkoa wa Arusha, Mrakibu Mwandamizi wa Polisi (SSP) Oscar Felician.





Na Mwandishi Wetu, Ilala

Mkuu wa Wilaya ya Ilala, mkoani Dar es Salaam, Edward Mpogolo, ametoa onyo kali kwa wakandarasi wote wanaotekeleza miradi ya ujenzi wa barabara wilayani humo, akiwataka kuzingatia mikataba na kukamilisha kazi kwa wakati.

Onyo hilo amelitoa wakati wa ziara ya ukaguzi wa miradi mbalimbali ya barabara, aliyoifanya kwa kushirikiana na baadhi ya wajumbe wa Kamati ya Usalama ya Wilaya, ambapo alitembelea miradi inayotekelezwa na wakandarasi, wengi wao wakiwa makampuni ya wazawa.

Akizungumza katika ziara hiyo, Mpogolo aliwakosoa baadhi ya wakandarasi kwa kuchelewesha miradi kwa visingizio visivyo na msingi, hali inayosababisha usumbufu kwa wananchi huku Serikali ikiwa tayari imeshatoa fedha kwa ajili ya utekelezaji wa kazi hizo.

Aidha, alionya tabia ya baadhi ya wakandarasi kukaidi maelekezo ya wasimamizi wa miradi kutoka TARURA na TANROADS, wakitumia mwanya wa kufahamiana na baadhi ya viongozi wa juu. Alisisitiza kuwa vitendo hivyo havitavumiliwa, hasa pale vinapoambatana na ujenzi wa barabara chini ya viwango vilivyokubaliwa kwenye mikataba.

Mpogolo, pia alieleza wasiwasi wake juu ya wakandarasi wanaochukua miradi mingi kwa wakati mmoja bila kuwa na uwezo wa kutosha wa rasilimali na vifaa, jambo linalosababisha baadhi yao kutelekeza miradi au kuchelewesha utekelezaji wake.

Kutokana na hali hiyo, aliagiza taasisi zote zinazohusika na usimamizi na uchunguzi wa miradi kuchukua hatua kali dhidi ya wakandarasi wanaokiuka taratibu na kushindwa kutekeleza majukumu yao ipasavyo katika Wilaya ya Ilala.

Katika ziara hiyo, Mpogolo, alitaja baadhi ya barabara zilizokaguliwa kuwa ni pamoja na Halisi na Kimanga, zilizogharimu shilingi bilioni 1.7 zilizotolewa mwaka 2024.

Barabara nyingine ni Mafia, Masasi, Magila, Bondi na Muhonda, zilizogharimu shilingi bilioni 1.8 zilizotolewa mwaka 2025.

Pamoja na barabara za Mwanza, Livingstone, Nyamwezi, Kipati, Msikitini, Sharifushamba, Kigoma na Tunduru, zilizogharimu shilingi bilioni 1.9.

Mpogolo alisisitiza kuwa Serikali haitavumilia uzembe wowote utakaoathiri ubora na kasi ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo inayolenga kuboresha miundombinu na maisha ya wananchi.













 

Timu ya Mpira wa Miguu ya Mashtaka imeshindwa kuonesha ubabe wake baada ya kukubali kichapo cha mabao 4-2 kutoka kwa TCDC Sports Club katika mechi ya kirafiki iliyochezwa kwenye Uwanja wa Venite, Mji Mwema mkoani Njombe.

Katika mchezo huo uliokuwa na ushindani mkubwa, TCDC Sports Club ilianza kwa kasi na kuonyesha kiwango bora tangu dakika za mwanzo. Kipindi cha kwanza kilishuhudia TCDC ikienda mapumziko ikiwa mbele kwa mabao 2-1, huku Mashtaka wakijitahidi kusawazisha bila mafanikio makubwa.

Kipindi cha pili kiliendelea kuwa na ushindani mkali, lakini TCDC waliendelea kutawala mchezo kwa kuongeza mabao mawili zaidi, wakionyesha umakini mkubwa katika safu yao ya ushambuliaji.

Mashtaka walifanikiwa kupata bao moja la kufutia machozi, lakini halikutosha kuzuia ushindi wa TCDC, na hivyo mchezo kumalizika kwa mabao 4-2.

Ushindi huo unaipa TCDC Sports Club morali kubwa wanapoendelea na maandalizi yao kupitia mechi za kirafiki dhidi ya timu mbalimbali za Wizara na Taasisi.

Mechi hizo ni sehemu ya kujiandaa kuelekea kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani (Mei Mosi) mwaka 2026, yatakayofanyika kitaifa mkoani Njombe.

Kwa upande wao, Mashtaka watalazimika kujipanga upya na kurekebisha mapungufu yaliyojitokeza ili kuimarisha kikosi chao katika michezo ijayo.



Na Mwandishi Wetu, Kaliua – Tabora


Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) kupitia Kituo cha Uzalishaji Mbegu za Miti, umeshiriki uzinduzi wa Maonesho ya Jukwaa la Tatu la Maendeleo ya Ushirika yanayofanyika wilayani Kaliua, mkoani Tabora, huku ukitumia jukwaa hilo kuhamasisha uhifadhi wa misitu na matumizi endelevu ya rasilimali za asili.

Maonesho hayo yamezinduliwa Aprili 29, 2026 na yanatarajiwa kuhitimishwa leo Aprili 30, 2026, yakibeba kaulimbiu isemayo “Linda Ushirika, Chagua Uadilifu”, ikiwa ni wito kwa wadau kuimarisha misingi ya uwajibikaji na usimamizi bora wa vyama vya ushirika.

Akizungumza katika uzinduzi huo kwa niaba ya Mkuu wa Kituo cha Uzalishaji Mbegu za Miti, Mhifadhi Medard Nogorya alieleza kuwa ushiriki wa TFS unalenga kusogeza huduma kwa wananchi pamoja na kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa upandaji miti na uhifadhi wa misitu katika kukuza uchumi wa jamii.

Katika hafla hiyo, Mkuu wa Wilaya ya Kaliua, Mheshimiwa Gerald Mongella, alipata fursa ya kutembelea banda la TFS na kupatiwa maelezo kuhusu shughuli za uzalishaji na usambazaji wa mbegu bora za miti, pamoja na mchango wake katika kuimarisha sekta ya misitu nchini.

Sambamba na maonesho hayo, TFS ilitumia pia vyombo vya habari kuifikia jamii kwa upana zaidi, ambapo ilitoa elimu ya uhifadhi kupitia kituo cha redio cha CG FM kinachosikika mkoani Tabora na wilaya zake, hatua inayolenga kuongeza mwamko wa wananchi kushiriki kikamilifu katika kulinda rasilimali za misitu.

Ushiriki wa TFS katika maonesho hayo ni sehemu ya mkakati mpana wa kuimarisha uhusiano na wadau, kukuza uelewa wa jamii kuhusu uhifadhi, na kuhamasisha matumizi sahihi ya rasilimali za misitu kwa maendeleo endelevu.











Top News