Na Janeth Raphael - MichuziTv

Wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Wasichana Mrijo Juu iliyopo wilayani Chemba mkoani Dodoma wamepata nafuu ya changamoto zinazowakabili wakati wa hedhi baada ya kupatiwa msaada wa vifaa maalumu vinavyoweza kutumika kwa muda mrefu, hatua inayolenga kuwawezesha kuendelea na masomo bila kukatishwa tamaa au kukosa vipindi vya darasani.

Msaada huo umetolewa na TotalEnergies Tanzania kwa kushirikiana na mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP), ukiwa sehemu ya juhudi za kuimarisha elimu ya mtoto wa kike na kuhakikisha anabaki shuleni hadi kukamilisha masomo yake.

Kila mwanafunzi alinufaika na kifurushi chenye taulo za kike zinazoweza kufuliwa na kutumika tena kwa muda wa zaidi ya miaka mitatu, pamoja na sabuni, nguo za ndani na ndoo kwa ajili ya kusaidia usafi na uhifadhi wa vifaa hivyo. Vifaa hivyo vinalenga kupunguza changamoto za upatikanaji wa pedi za mara kwa mara pamoja na kusaidia usafi wa mazingira.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi wa Sheria na Uhusiano wa TotalEnergies Tanzania, Detrude Mpangile, amesema taulo hizo zimeundwa kwa ubora wa juu na zinaweza kumhudumia mwanafunzi kwa kipindi chote cha elimu ya sekondari kuanzia kidato cha kwanza hadi cha nne. Alibainisha kuwa mpango huo pia unachangia utunzaji wa mazingira kutokana na kupunguza taka zinazotokana na pedi za kutupwa mara moja.

Kwa upande wake, Mtaalamu na Msimamizi wa Miradi ya Uwekezaji na Uwajibikaji kutoka EACOP, Mhandisi Peter Kiungai, amesema mpango huo uliozinduliwa Machi mwaka huu ni sehemu ya mwendelezo wa kurudisha kwa jamii, ukiwa na lengo la kuhakikisha wasichana wanapata mazingira bora ya kusoma bila vikwazo vinavyotokana na changamoto za hedhi.

Akimwakilisha uongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Chemba, Regina Bahaye aliishukuru kampuni ya TotalEnergies Tanzania na EACOP kwa kuendelea kuwafikia wanafunzi na kuwapatia msaada huo, akisisitiza kuwa hatua hiyo itasaidia kupunguza utoro shuleni na kuongeza umakini darasani kwa wanafunzi wa kike.

Kwa niaba ya wanafunzi wenzake, Scolastica amesema msaada huo umewaletea faraja kubwa kwani utawasaidia kuhudhuria masomo kwa utulivu zaidi wakati wa hedhi, huku ukipunguza mzigo wa gharama kwa wazazi na kuchangia utunzaji wa mazingira kutokana na matumizi ya taulo zinazoweza kufuliwa na kutumika tena.

Msaada huo unaendelea kuonekana kuwa sehemu muhimu ya jitihada za kuinua elimu ya mtoto wa kike katika wilaya ya Chemba, ukilenga kuhakikisha hakuna mwanafunzi anayekosa masomo kutokana na changamoto za kibaolojia zinazoweza kudhibitiwa.





Na Janeth Raphael MichuziTv 

Serikali imewataka wakulima na wadau wote wa zao la pareto nchini kuweka mkazo katika uzalishaji wenye ubora ili kuongeza ushindani wa zao hilo kwenye soko la kimataifa na kuinua mchango wake katika uchumi wa taifa.

Wito huo umetolewa na Naibu Waziri wa Kilimo, David Silinde, wakati akifungua Mkutano Mkuu wa 16 wa Wadau wa Zao la Pareto uliofanyika Juni 26, 2026, jijini Dodoma

Silinde amesema maendeleo ya sekta ya pareto yanategemea uzalishaji unaokidhi viwango vya ubora, huku akisisitiza wadau kutumia mkutano huo kuweka mikakati ya kuongeza uzalishaji kutoka tani 3,800 zilizozalishwa mwaka 2025/2026 hadi kufikia lengo la tani 9,000 kwa mwaka.

Aidha, amewataka wadau kuboresha ubora wa maua ya pareto kwa kuzingatia viwango vinavyohitajika sokoni, ikiwemo kuongeza kiwango cha kirutubisho cha asili cha pyrethrin, ambacho ndicho kinacholipa thamani kubwa zao hilo katika biashara ya kimataifa.

Kwa mujibu wa Silinde, pareto ni moja ya mazao ya kimkakati yanayoendelea kuingizia Tanzania fedha za kigeni, ambapo kwa sasa mauzo yake nje ya nchi yanaingiza takribani Dola za Marekani milioni 9, sawa na zaidi ya Shilingi bilioni 23.4 kwa mwaka.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Nafaka na Mazao Mchanganyiko (COPRA), Irene Mlola, amesema mamlaka hiyo tayari imeanza kusambaza vifaa vya kudhibiti unyevu wa pareto katika halmashauri 17 zinazolima zao hilo, hatua inayolenga kulinda ubora wa mazao baada ya kuvunwa.

Ameongeza kuwa katika kipindi kifupi kijacho, COPRA itaanza ujenzi wa vituo vya kukaushia pareto ili kupunguza upotevu wa ubora na kuongeza thamani ya zao hilo kabla ya kuingia sokoni.

Mlola amesema mkutano huo pia unajadili namna ya kuwashirikisha vijana zaidi katika mnyororo wa thamani wa pareto kupitia uzalishaji wa mbegu bora, shughuli za ugani, usindikaji pamoja na maeneo mengine ya biashara yanayohusiana na zao hilo.

Mkutano huo umehudhuriwa na wakulima wa pareto kutoka maeneo mbalimbali nchini, wakurugenzi wa halmashauri zinazozalisha zao hilo, viongozi wa serikali, maafisa ugani pamoja na wadau wengine wa sekta hiyo.

Katika hafla hiyo, Naibu Waziri David Silinde alimwakilisha Waziri wa Kilimo, Daniel Chongolo, ambaye alikuwa na majukumu mengine ya kitaifa.







-Wanaume 14 tayari mambo yao safi, daktari aeleza hatua zote muhimu


Na Said Mwishehe,Michuzi TV-Dodoma


HOSPITALI ya Benjamin Mkapa imesema gharama za huduma ya upandikizaji wa uume katika hospitali hiyo ni Sh.milioni 10, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kusaidia wanaume wenye changamoto za kiafya zinazohusiana na nguvu za kiume kurejesha furaha ya ndoa.

Akizungumza na Wahariri wa vyombo vya habari waliotembelea hospitali hiyo na kushuhudia mafanikio lukuki ya utoaji huduma, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa hospitali hiyo, Dkt. Abdallah Baja amesema huduma ya kupandikiza uume inafanyika katika hospitalini hapo peke yake.

“Tumekuwa tukitoa huduma hii ya kupandikiza uume tangu mwaka 2023 na huduma hii ni sehemu ya huduma za kibingwa na kibingwa bobezi tunazozitoa zaidi ya 20.”

Amefafanua hospitali hiyo iliamua kuanzisha huduma hiyo baada ya kubaini kuwepo kwa changamoto kubwa miongoni mwa wanaume wengi, hali iliyosababisha baadhi yao kutafuta suluhisho kupitia waganga wa kienyeji na dawa zinazodaiwa kutibu tatizo hilo.

“Tuliona umuhimu wa kuja na mkakati wa kuwasaidia watu wenye changamoto za nguvu za kiume. Kwa maana hiyo, tulianza kutoa huduma hii na hadi sasa wanaume 14 wamepandikizwa uume.”

Ameongeza baada ya kufanyiwa matibabu hayo, wanaume hao walitoa mrejesho mzuri kuhusu hali zao na kwamba walipewa maelekezo ya kuanza kushiriki tendo la ndoa baada ya wiki sita tangu kufanyiwa upasuaji.

“Hizo ni taarifa kutoka kwao wenyewe kwa sababu tuliendelea kuwafuatilia. Wametueleza kuwa hali zao ni nzuri na wamefurahi kwa kuwa uwezo wao umerudi, jambo ambalo limewarejeshea heshima katika familia zao,” amesema Dkt. Baja.

Ameongeza kwamba hospitali hiyo ipo katika mkakati wa kupanua huduma hiyo ili iweze kuwafikia watu wengi zaidi wanaohitaji matibabu hayo.

“Kinachofanyika si kuweka uume bandia bali uume wako tupandikiza vitu vya kuamsha msuli na baada ya kufanyiwa upasuaji unarudi katika hali yako ya kawaida na unakuwa hadi mwisho wa uhai wako,” amesema.









Na Said Mwishehe,Michuzi TV-Dodoma

HOSPITALI ya Benjamin Mkapa iliyopo jijini Dodoma imesema inajivunia mafanikio makubwa ambayo imeendelea kuyapata katika utoaji huduma za afya za kibingwa na Ubungo’s bobezi.

Hayo yamesemwa leo Juni 25,2026 na Kaimu Mkurugenzi Mtendaji Mkuu wa Hospitali ya Benjamin Mkapa, Abdallah Baja wakati wa kikao kazi kati ya hospitali hiyo na Wahariri wa vyombo vya habari ambao ni wanachama wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) linaloongozwa na Mwenyekiti wake Deodatus Balile.

Akieleza zaidi amesema hospitali hiyo mwaka 2025 ilitangazwa kuwa hospitali bora zaidi nchini katika kundi la hospitali za rufaa za kanda kwa ubora wa huduma za afya, ikiibuka kinara mbele ya hospitali nyingine kubwa nchini zikiwemo Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Mbeya na KCMC.

Aidha, amesema Waziri wa Afya Mohammed Mchengerwa aliwahi kuzielekeza hospitali zote nchini kujifunza kutoka Hospitali ya Benjamin Mkapa kuhusu namna bora ya kuwahudumia wagonjwa, jambo linalothibitisha kiwango cha juu cha huduma zinazotolewa na hospitali hiyo.

Baja alieleza Hospitali ya Benjamin Mkapa ilikuwa hospitali ya pili nchini kuanza huduma za upandikizaji wa figo, huku ikiwa hospitali ya kwanza Tanzania kufanya upandikizaji wa uume (Penile Transplant). Pia ni hospitali ya kwanza ya serikali kufanya upasuaji wa kisasa wa macho na ya pili nchini kufanya upasuaji wa moyo kwa watoto.

Kwa mujibu wa Baja, hospitali hiyo pia imekuwa ya kwanza nchini kutumia mfumo wa hospitali tembezi (Mobile Hospital), ambapo magari maalumu yenye vifaa vya upasuaji, makazi ya wataalamu na vifaa tiba hupelekwa kutoa huduma katika maeneo mbalimbali ndani na nje ya Tanzania. Alisema huduma hizo tayari zimefika katika nchi za Burundi na Malawi.

Akizungumzia historia ya hospitali hiyo, Baja amesema Hospitali ya Benjamin Mkapa ilianzishwa Oktoba 13, 2015 na ilianza na vitanda 40 lakini kwa sasa ina kufika vitanda 600 na inapokea wastani wa wagonjwa zaidi ya 1,200 kwa siku katika huduma za nje.

Ameongeza hospitali hiyo ina majukumu makuu manne ambayo ni utoaji wa huduma za afya, kinga na uhamasishaji wa afya, mafunzo kwa wanafunzi wa kada mbalimbali za afya, pamoja na kufanya tafiti kwa kushirikiana na taasisi za elimu ya juu.

“Tunapokea wanafunzi kutoka Chuo Kikuu cha Dodoma na vyuo vingine mbalimbali nchini kwa ajili ya mafunzo kwa vitendo. Ushirikiano wetu na taasisi za elimu na utafiti unatupa uwezo wa kuunganisha nadharia na vitendo kwa manufaa ya wagonjwa,” amesema Baja.

Ameongeza hospitali hiyo kwa sasa inatoa huduma za kibingwa na ubingwa bobezi, zikiwemo huduma za figo, upasuaji wa ubongo, moyo, mifupa na huduma nyingine za kisasa ambazo zimekuwa zikipatikana kwa kiwango cha kimataifa.

Baja ametumia fursa hiyo kuwakaribisha wananchi na wadau mbalimbali kutembelea Hospitali ya Benjamin Mkapa ili kujionea ubora wa huduma zinazotolewa, akisisitiza kuwa hospitali hiyo imeendelea kuwa nguzo muhimu katika kuboresha huduma za afya nchini.









Kamati ya Wataalam ya Serikali ya Maandalizi ya Mashindano ya Kombe la Mataifa Afrika mwaka 2027 (AFCON 2027) imeweka mkazo katika kuhakikisha miradi ya ujenzi na uboreshaji wa barabara inayotekelezwa kuelekea michuano hiyo inakamilika kwa wakati, ili kuboresha usafiri na usafirishaji.


Akifungua kikao kazi cha Kamati hiyo kilichofanyika Jijini Arusha tarehe 26 Juni, 2026, Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Arusha, Dkt. Charles Mkombachepa, amesema, Mkoa wa Arusha unaendelea kushuhudia utekelezaji wa miradi mingi ya barabara katika maeneo mbalimbali ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya AFCON 2027.

 Amesisitiza Kamati hiyo kujadili kwa kina na kuweka mikakati madhubuti ya kufuatilia utekelezaji na ukamilishaji wa miradi hiyo, hususan katika maeneo na vituo vitakavyotumika wakati wa mashindano.

Awali, Mkurugenzi wa  Maendeleo ya Michezo, Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Bw. Boniface Tamba, amesema Kamati hiyo ina jukumu la kuratibu, kufuatilia na kuhakikisha utekelezaji wa miradi yote ya maandalizi ya AFCON 2027 inafanyika kwa ufanisi na kwa kuzingatia muda uliopangwa.

Kamati hiyo, inaundwa na wajumbe kutoka wizara na taasisi mbalimbali za Serikali,ikiwa na lengo la kuimarisha uratibu wa maandalizi na kuhakikisha Tanzania inakuwa tayari kuandaa kwa mafanikio michuano hiyo mikubwa Afrika.









 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, akizungumza na ujumbe wa Kampuni ya Heidelberg Materials, ambao ni wazalishaji wa Saruji chapa ya Simba Cement na Twiga Cement, ulioongozwa na Mjumbe wa Bodi ya Uongozi na Mtendaji Mkuu wa Afrika, Mediterranean na Asia Magharibi, Bw. Hakan Gurdal, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 26 Juni, 2026
 
Katika mazungumzo hayo, Kampuni hiyo imewasilisha mpango wa kupanua uwekezaji wake nchini, ukiwemo kuongeza uzalishaji wa Saruji, matumizi ya nishati safi na mradi wa usindikaji wa taka za majiji kwa ajili ya uzalishaji.






 

-Yatoa mwaka mmoja ili waweze kujiimarisha

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali imetoa msamaha wa kodi ya mapato kwa kwa kipindi cha mwaka mmoja kwa wafanyabiashara wadogo ambao ni wapya ili waweze kujiimarisha katika biashara wanazozianzisha.

“Ili kuwavutia wajasiriamali, Serikali itatoa msamaha wa kodi ya mapato kwa wafanyabiashara wadogo ambao ni wapya kwa kipindi cha mwaka mmoja tangu tarehe ya kupata namba ya utambulisho wa mlipakodi,” amesema. 

Amesema hatua hiyo itawawezesha akinamama lishe na baba lishe, waendesha bodaboda na bajaji, mafundi seremala na wachomeleaji na wengine wenye shughuli ndogondogo kuanzisha biashara zao bila kuwa na changamoto ya kudaiwa kodi ndani ya mwaka mmoja, na kwamba muda huo utatoa fursa ya kujiimarisha katika biashara wanazozianzisha.

Ametoa kauli hiyo bungeni jijini Dodoma leo (Ijumaa, Juni 26, 2026) wakati akielezea maeneo yaliyofanyiwa maboresho ya kodi katika hotuba ya kuhitimisha mkutano wa tatu wa Bunge. Bunge limeahirishwa hadi Agosti 25, mwaka huu.

Akielezea eneo jingine ambalo limewekewa nafuu ya kikodi, Waziri Mkuu amesema Serikali itasamehe kodi kwenye vifaa vitakavyotumika katika vituo vya kuchaji magari yanayotumia umeme na kupunguza ushuru wa forodha kutoka asilimia 25 hadi asilimia 10. Aidha, amewataka wadau wa sekta binafsi watumie fursa hiyo kuagiza mashine na vipuri vitakavyotumika kwenye vituo hivyo.

Akielezea azma ya Serikali kuimarisha mtiririko wa fedha katika mifuko ya miradi ya maendeleo, Dkt. Mwigulu amesema wa sasa asilimia 70 ya fedha za mifuko ya maendeleo zitaelekezwa moja kwa moja kwenye mifuko husika ili uweze kutekeleza majukumu yake ya kimsingi.

Amesema uamuzi huo utaongeza kasi na uhakika wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kupanua wigo wa huduma za jamii na kuongeza fursa za uzalishaji. Uamuzi huo unatokana na ushauri uliotolewa na Wabunge kwa Serikali wakiitaka ichukue hatua za haraka kuwezesha sekta mbalimbali ikiwemo maji, barabara na umeme zinapata fedha kwa wakati.

“Nitumie fursa hii kuwakumbusha watendaji wa taasisi ambazo zitapelekewa fedha hizo, wahakikishe wanakamilisha miradi iliyokusudiwa, tena kwa kuzingatia thamani ya fedha na miradi iwe na uimara. Wakumbuke kuwa dhamira na maelekezo ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ni kutekeleza kikamilifu miradi ya maendeleo kwa ajili ya ustawi wa Watanzania,” amesisitiza.

Akitoa mwelekeo wa bajeti na vipaumbele vya sekta kwa mwaka 2026/2027, Dkt. Mwigulu amesema vipaumbele vya kila wizara za kisekta vimezingatia maslahi mapana ya Taifa na kwamba bajeti ijayo itaendelea kuimarisha uwekezaji katika sekta za uzalishaji, miundombinu na huduma za jamii. 

“Serikali imejipanga kuendelea kuimarisha mifumo ya mapato ya ndani na kupunguza utegemezi wa mikopo na misaada kutoka nje. Mkakati mmojawapo ni kupunguza utegemezi kutoka nje,” amesisitiza.

Amesema bajeti hiyo inaenda kuweka mazingira wezeshi ya kuvutia urasimishaji wa sekta isiyo rasmi ambayo inaajiri zaidi vijana na wanawake. Kupitia utaratibu mpya wa utoaji mikopo inayotokana na asilimia 10 ya mapato ya ndani ya halmashauri, Waziri Mkuu amezielekeza taasisi za fedha na waratibu wa mikopo hiyo kuondoa masharti magumu yanayokwamisha wajasiriamali kunufaika na mikopo hiyo. 

“Mfano ni ulazima wa wahitaji kwa upande wa watu wenye ulemavu kutakiwa kuunda vikundi na ulazima wa wahitaji kuwasilisha dhamana kubwa kama vile hati za nyumba ambavyo kwa asili ya biashara zao, hawawezi kuwa navyo,” amesisitiza.



Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Angellah Jasmine Kairuki (Mb) afungua kikao cha majadiliano kuhusu DPI for Inclusive Growth katika Wiki ya Kimataifa ya Teknolojia Huria (UN Open Source Week 2026) jijini New York, Marekani. 

Tanzania ni miongoni mwa nchi zilizoandaa maadhimisho hayo yanayohudhuriwa na mataifa na wadau mbalimbali wa teknolojia ulimwenguni. 

Katika hotuba yake ya ufunguzi Waziri Kairuki alisema Tanzania imepiga hatua katika ujenzi wa mifumo ya kidijitali ikiwemo utambuzi wa kidijitali, mifumo ya malipo na mifumo ya kubadilishana taarifa kati ya sekta mbalimbali, ambayo ni msingi wa mageuzi ya kidijitali na utoaji wa huduma bora kwa wananchi.

Waziri Kairuki amesema Serikali chini ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuimarisha miundombinu ya kidijitali kupitia Mkongo wa Taifa wenye zaidi ya kilomita 27,000 za nyuzi za mawasiliano, vituo vya kuhifadhi data na mifumo inayounganisha taasisi za umma na binafsi.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa ushirikiano wa kimataifa katika matumizi ya teknolojia huria ili kuimarisha ubadilishanaji wa taarifa, usalama wa mtandao na matumizi salama ya Akili Unde (AI), akieleza kuwa hakuna nchi wala mwananchi anayepaswa kuachwa nyuma katika safari ya uchumi wa kidijitali.





Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi amesema Watanzania wataanza kushuhudia kushuka kwa bei za mafuta kuanzia mwezi Julai mwaka huu kufuatia kuanza kushuka kwa bei ya mafuta ghafi katika soko la dunia baada ya kusitishwa kwa mapigano ya Mashariki ya Kati.

Akijibu mwongozo wa Mbunge wa Jimbo la Bagamoyo na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Mhe. Subira Mgalu, Bungeni jijini Dodoma leo, Juni 26, 2026, Waziri Ndejembi amesema Serikali imezielekeza EWURA, TPDC na PBPA kuhakikisha manufaa ya kushuka kwa bei za mafuta katika soko la dunia yanawafikia walaji nchini.

Amesema licha ya athari za vita kati ya Iran, Israel na Marekani zilizosababisha usumbufu katika usafirishaji wa mafuta kupitia Mlango wa Hormuz, Tanzania iliendelea kuwa na uhakika wa upatikanaji wa mafuta bila kukumbwa na uhaba.

Ndejembi amesema hatua za haraka zilizochukuliwa na Serikali zilihakikisha mafuta yanapatikana katika maeneo yote ya nchi, huku Tanzania ikiendelea kuwa miongoni mwa nchi zenye bei nafuu za mafuta katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Ameeleza kuwa baada ya makubaliano ya kusitisha mapigano, bei ya mafuta ghafi imeanza kushuka hadi kufikia takribani dola 70 kwa pipa, hali inayotarajiwa kuleta nafuu katika soko la ndani kadri shehena mpya zilizonunuliwa kwa bei ya chini zitakavyoingia nchini.

“Watanzania wataanza kuona punguzo la bei kuanzia mwezi Julai, na kadri shehena mpya za mafuta zilizonunuliwa kwa bei nafuu zitakavyoendelea kuwasili nchini, ndivyo bei zitakavyozidi kushuka,” amesema Waziri Ndejembi.

Aidha, amesema wataalamu wa soko la dunia wanatarajia ndani ya wiki nane hadi 10 bei za mafuta kurejea katika viwango vilivyokuwepo kabla ya kuanza kwa mgogoro huo mwezi Februari mwaka huu.

Waziri Ndejembi ameongeza kuwa Serikali itaendelea kufuatilia mwenendo wa soko la dunia huku ikiimarisha mikakati ya muda mrefu ya kuhakikisha upatikanaji wa mafuta nchini, ikiwemo kuongeza vyanzo vya uagizaji wa mafuta na kuharakisha utekelezaji wa mpango wa ujenzi wa kiwanda cha kusafisha mafuta mkoani Tanga ili kuimarisha usalama wa nishati nchini. 



 

Mamlaka ya Majisafi na usafi wa Mazingira Tanga (Tanga UWASA) imepokea ugeni wa viongozi wa kanda na wawakilishi kutoka Mfuko wa Umoja wa Mataifa wa Maendeleo ya Mitaji (UNCDF) ukiongozwa na Katibu Mtendaji wa Mfuko huo Bw. Pradeep Kurukulasuriya uliolenga kutembelea na kujionea maendeleo ya utekelezaji wa Mradi wa kuboresha hali ya upatikanaji huduma ya maji Tanga awamu ya tatu kupitia ufadhili wa Hatifungani ya Kijani ambapo UNCDF ni miongoni mwa wadau muhimu walioshiriki katika hatua za awali za kufanikisha mradi huo.

Katika ziara hiyo, Katibu Mtendaji na wageni walipokea taarifa ya mradi na mwenendo wa magawio kwa wawekezaji pamoja na kutembelea eneo la mradi na kujionea kasi ya utekelezaji wa shuguli mbalimbali zinazolenga kuongeza na kuimarisha upatikanaji wa huduma ya maji ya uhakika kwa wakazi wa maeneo ya kihuduma ya Tanga UWASA unaotarajiwa kukamilika mapema mwezi Agosti, 2026.

Katibu Mtendaji pamoja na wageni walipata pia fursa ya kufanya kikao na sehemu ya wanufaika wa mradi wa Hatifungani katika Hospiali ya Jiji iliyopo kata ya Masiwani ambapo awali walikuwa wakipata changamoto katika kutoa huduma kutokana na adha ya upatikanaji wa huduma ya maji ya uhakika na kupitia mradi wa Hatifungani wameboreshewa miundombinu hivyo kuimarisha upatikanaji wa uhakika wa huduma ya majisafi.

Akizungumza mara baada ya ziara hiyo, Katibu Mtendaji wa UNCDF Bw. Pradeep Kurukulasuriya  ameipongeza Tanga UWASA kwa uthubutu huo na kwa maendeleo mazuri ya utekelezaji wa mradi lengwa sambamba na kuonesha nia ya kuongeza wigo wa kuendelea kushirikiana.


" Tunajivunia kuwa sehemu ya mchango katika kufanikisha Hatifungani ya Kijani ya Tanga na matarajio yetu ni kwamba mradi huu utaboresha maisha ya jamii na kupitia hili Tanga UWASA imedhihirisha kuwa inawezekana kuhamasisha uwekezaji ndani ya nchi kwani takriban asilimia 65 ya uwekezaji ulitoka kwa wawekezaji wa Kitanzania, na kwa kupitia mpango huu, tumedhihirisha kuwa mitaji ya ndani inaweza kuhamasishwa ili kufadhili miradi muhimu ya maendeleo na kwa sasa tunasoma mfano huu kwa karibu, tunatafuta kuelewa ni nini kilifanya kazi vizuri, changamoto zipi zilizojitokeza, na ni somo gani tunaweza kujifunza ili tuweze kuiga mafanikio ya Hatifungani ya Tanga si tu ndani ya Tanzania bali katika nchi nyingine pia", alisema Bw. Kurukulasuriya.

Awali kabla ya ziara hiyo, Katibu Mtendaji wa UNCDF na wageni wakiongozwa na Kaimu Mkurugenzi wa Tanga UWASA, Eng. Salum Ngumbi walifika katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Tanga kutoa salamu na kupokelewa na Mkuu wa Wilaya ya Tanga Mhe. Dadi Kolimba aliyetoa salamu za Mkoa kwa niaba ya Mhe. Balozi Dkt. Batilda Salha Buriani Mkuu wa Mkoa wa Tanga







Top News