Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Mauritius, Kamishna wa Polisi (CP) Suzan Kaganda, mwenye makazi yake ya kikazi Jijini Harare, Zimbabwe, amewasilisha Hati za Utambulisho kwa Rais wa Jamhuri ya Mauritius, Mhe. Dharambeer Gokhool, katika hafla iliyofanyika Julai 6, 2026, Ikulu ya Serikali iliyopo Reduit, Mauritius.

Baada ya kuwasilisha hati hizo, Balozi Kaganda alifanya mazungumzo na Mheshimiwa Rais Gokhool, ambaye alimpongeza kwa uteuzi wake na kumkaribisha rasmi katika eneo lake la uwakilishi, huku Rais huyo pia akimhakikishia ushirikiano na Serikali ya Mauritius katika kipindi chote cha utekelezaji wa majukumu yake ya kidiplomasia.

Kwa upande wake, Balozi Kaganda alishukuru kwa mapokezi mazuri aliyopatiwa na kuahidi kuendeleza ushirikiano wa karibu na Serikali ya Mauritius katika kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia kati ya Tanzania na Mauritius ambapo aliweka wazi kuwa dhamira yake ni kuendeleza ushirikiano katika sekta za biashara, uwekezaji, utalii na Uchumi wa Buluu kwa manufaa ya wananchi na maendeleo ya nchi hizo mbili.

Balozi (CP) Kaganda pia anaiwakilisha Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Zimbabwe, akiwa na makazi ya kikazi jijini Harare.






📍NIRC: DODOMA

Tume ya Taifa ya Umwagiliaji (NIRC) imeanza kuweka mikakati ya jinsi ya kusafirisha mitambo yake mikubwa ya kuchimba visima virefu kwenda maeneo mbalimbali nchini, hususani yale yenye changamoto kubwa ya upatikanaji wa maji chini ya ardhi, mara baada ya kukamilisha kazi katika shamba la Chinangali.

Mkurugenzi Mkuu wa NIRC, Raymond Mndolwa, ametoa agizo hilo kwa Idara ya Mitambo, ya Tume hiyo kutathmini namna bora ya kusafirisha mitambo hiyo bila kuathiri miundombinu ya barabara kutokana na uzito wake mkubwa.

“Tuone namna bora kwa Idara husika kushauri kama tunaweza kusafirisha mitambo hii nusu nusu (kwa kuifungua) kutokana na uzito wake, ili isiathiri barabara zetu inapokwenda mikoa tofauti,” amesisitiza Mndolwa.

Agizo hilo amelitoa wakati wa ziara yake katika shamba la vijana la mradi wa Jenga Kesho Iliyo Bora (BBT) lililopo Chinangali mkoani Dodoma.

Ziara hiyo ililenga kukagua maendeleo ya ujenzi wa barabara za ndani, mabwawa,uchimbaji wa visima na uwekaji wa miundombinu ya Umwagiliaji katika mashamba hayo,inayotekelezwa na Tume hiyo.

Katika ziara hiyo, Mndolwa alikagua mtambo huo wa kisasa wenye uwezo wa kuchimba visima virefu hadi mita 1,800 chini ya ardhi, ambao kwa sasa upo Chinangali kwa ajili ya kuchimba visima viwili vya mwisho. Visima hivyo vitakamilisha jumla ya visima 40 vinavyochimbwa na NIRC shambani hapo, sambamba na mabwawa matatu ambapo mawili tayari yamekamilika ili kuongeza kasi ya upatikanaji wa maji.

Mndolwa aliambata na wataalamu mbalimbali akiwemo Mkurugenzi wa Idara ya Uendelezaji Miundombinu Mhandisi Leopard Runji, Mhandisi wa Mkoa wa Dodoma Oswald Urassa na Muendesha Mitambo hiyo ya Visima virefu Mosses Mkude. 







Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) umeendelea kuimarisha juhudi za kupanua wigo wa hifadhi ya jamii nchini kwa kuwahamasisha wananchi waliojiajiri kujiunga na Hifadhi Skimu, huku ukiwahimiza waajiri wenye malimbikizo ya michango kunufaika na msamaha wa tozo uliotolewa na Mfuko. Wito huo umetolewa wakati wa Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba).

Akizungumza baada ya kutembelea banda la NSSF katika maonesho hayo, Mkurugenzi Mkuu wa NSSF, Bw. Masha Mshomba, alisema ameridhishwa na mwitikio wa wananchi pamoja na huduma zinazotolewa na Mfuko, hususan elimu kuhusu hifadhi ya jamii, usajili wa wanachama wapya na huduma za kidijitali.

Bw. Mshomba alisema banda la NSSF limeendelea kuwa jukwaa muhimu la kutoa elimu kwa wananchi kuhusu nafasi ya hifadhi ya jamii katika kuboresha ustawi wa maisha, kupunguza umaskini, kuimarisha nguvu kazi na kuongeza uzalishaji katika uchumi wa taifa.

Kupitia Hifadhi Skimu, alisema wananchi waliojiajiri wanaweza kujiunga na NSSF kwa hiari na kuchangia kwa viwango vinavyolingana na uwezo wao.

Alieleza kuwa kiwango cha chini ni shilingi 30,000 kwa mwezi kinachomwezesha mwanachama kupata huduma za matibabu, huku mchango wa shilingi 52,200 ukimpa mwanachama huduma za matibabu yeye mwenyewe, mwenza wake na watoto wasiozidi wanne.

Alifafanua kuwa wanachama wa skimu hiyo pia hunufaika na mafao ya uzazi, ulemavu, pensheni ya uzee na urithi, akibainisha kuwa mfumo huo unaruhusu michango kufanyika hata kila siku ilimradi ifikie kiwango cha mwezi.

Bw. Mshomba alisema mafanikio hayo yametokana na maboresho ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambayo yameongeza ushiriki wa wananchi waliojiajiri katika mfumo rasmi wa hifadhi ya jamii.

Katika huduma za kidijitali, alisema NSSF imeboresha mifumo yake inayowezesha wanachama na waajiri kujihudumia popote kupitia NSSF Portal bila kufika ofisini, hatua iliyorahisisha upatikanaji wa huduma kwa wakati.

Katika hatua nyingine, Bw. Mshomba alisema NSSF imetoa msamaha wa tozo kwa waajiri wenye madeni ya michango kuanzia Juni hadi Desemba 2026, ili kuwapa fursa ya kulipa madeni ya msingi na kupunguza mzigo wa tozo.

Alisema waajiri watakaolipa madeni yao ya msingi kuanzia Juni hadi Agosti 31, 2026 watanufaika na msamaha wa asilimia 100 ya tozo, mradi waendelee kulipa michango ya sasa kwa wakati hadi Januari 2027. Wataakaoanza kulipa kati ya Septemba 1 na Oktoba 31 watanufaika na msamaha wa asilimia 75, huku watakaoanza kulipa kati ya Novemba 1 na Desemba 31 wakinufaika na msamaha wa asilimia 50.

Aliwataka waajiri kutumia fursa hiyo kuongeza tija katika uzalishaji badala ya kuelekeza rasilimali katika kulipa tozo, huku akisisitiza umuhimu wa kuwasilisha michango kwa wakati ili kulinda haki za wafanyakazi.

Pia aliwahimiza waajiriwa kufuatilia michango yao na kutoa taarifa NSSF endapo michango yao haiwasilishwi kwa mujibu wa sheria.

Akizungumzia ukuaji wa Mfuko, Bw. Mshomba alisema thamani ya NSSF imeongezeka kutoka shilingi trilioni 4.8 mwezi Machi 2021 hadi shilingi trilioni 9.8 kufikia Juni 30, 2026 kwa mujibu wa hesabu zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), huku hesabu ambazo bado hazijakaguliwa katika mwaka wa fedha ulioishia Juni 30, 2026, zikionesha thamani ya zaidi ya shilingi trilioni 11.6.

Alieleza kuwa ukuaji huo umetokana na ongezeko la michango, uwekezaji wenye tija pamoja na matumizi ya teknolojia katika utoaji wa huduma.

Kwa upande wa uwekezaji, alisema NSSF imeanza kuwekeza nje ya nchi baada ya kupata kibali kutoka Benki Kuu ya Tanzania (BoT), ikilenga masoko ya mitaji na miradi ya majengo ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), ikiwemo ujenzi wa majengo ya biashara jijini Nairobi, Kenya, yatakayoongeza mapato na kuimarisha uwezo wa Mfuko.









Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Mhe. Dkt. Rhimo Nyansaho, amewapongeza viongozi wa  Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) na Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) kwa juhudi wanazozifanya za kuimarisha ulinzi na usalama nchini.

Amesema hayo wakati akizungumza na waandishi wa habari kwenye maadhimisho ya miaka 50 ya biashara ya kimataifa jijini Dar es Salaam  Sabasaba, Julai 6, 2026, amesisitiza kuwa vyombo hivyo vya ulinzi vimekuwa vikiendelea kulinda amani ya nchi, jambo linalowezesha wananchi kufanya shughuli za maendeleo na kufanikisha utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya 2050.

Aidha amesema shirika  la JKT linafanya kazi za uzalishaji mali pamoja na kuwafundisha vijana, hatua inayosaidia kuwaandaa kujitegemea na kujiajiri.

Ameeleza kuwa kupitia maonesho hayo, taasisi hizo zimepata nafasi ya kuonesha shughuli mbalimbali zinazofanyika kwenye vikosi vyao, ikiwemo kutoa huduma kwa wananchi na mafunzo kwa vijana.

Amesema kampuni ya usafi na unyunyuzi dawa ya SUMA JKT ambayo imefanikiwa kuajiri vijana 4,800, hatua inayoonesha mchango wa taasisi hizo katika kupunguza changamoto ya ajira nchini.



Taasisi ya Tiba ya Mifupa na Ubongo (MOI) imesema itaendelea kuimarisha tafiti zinazolenga kuzalisha afua za matibabu zinazozingatia mazingira na vinasaba vya Watanzania, ili kuboresha huduma za matibabu ya magonjwa ya mifupa na mfumo wa fahamu.

Akizungumza na waandishi wa habari Mkurugenzi Mtendaji wa MOI, Balozi Dkt. Mpoki Ulisubisya, Jijini Dar es Salaam Julai 6, 2026, kwenye Maadhimisho ya Miaka 50 ya Maonesho ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba).

Amesema mara nyingi tiba zinazotumika hutokana na matokeo ya tafiti zilizofanyika katika nchi zilizoendelea pamoja na baadhi ya nchi za bara la Afrika, ambapo afua hizo zinaweza kuwa zimezingatia watu wenye vinasaba tofauti, hivyo wao wameona umuhimu wa kufanya tafiti zitakazozalisha afua zinazokidhi mazingira ya Tanzania.

Aidha, amesema MOI imetimiza miaka 30 tangu kuanzishwa kwake na imeendelea kujikita katika maeneo makuu matatu ambayo ni kutoa huduma kwa wagonjwa wa mifumo ya ubongo na mifupa, kufundisha huduma hizo kwa wananchi na wataalam katika ngazi ya shahada ya kwanza, shahada ya pili na ubobezi, pamoja na kufanya tafiti.

Pia amesema taasisi hiyo imeweza kutoa mafunzo kwa wananchi na wataalam kutoka ndani na nje ya Tanzania, hususan katika ukanda wa Afrika Mashariki, Kati, Kusini na Magharibi, ikiwa ni sehemu ya kuimarisha huduma za afya katika kanda hiyo.





📍Dar es Salaam

Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Dkt. Janet Lekashingo, amesema Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 imeipa sekta ya madini nafasi ya kimkakati ya kuongoza mageuzi ya uchumi wa Tanzania kupitia uongezaji thamani wa madini, ushirikishwaji wa watanzania na matumizi ya teknolojia za kisasa katika shughuli za uchimbaji wa madini.

Akizungumza mapema leo Julai 6, 2026, alipotembelea mabanda ya taasisi zilizo chini ya Wizara ya Madini katika Kijiji cha Madini kwenye Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), Dkt. Lekashingo amesema Tume ya Madini imejipanga kikamilifu kutekeleza malengo ya Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 ili sekta ya madini iwe nguzo muhimu ya ukuaji wa uchumi na maendeleo endelevu.

Amesema utekelezaji wa dira hiyo unalenga kuongeza thamani ya madini ndani ya nchi badala ya kuyasafirisha ghafi, kuimarisha utafiti wa jiolojia ili kubaini maeneo mapya yenye rasilimali za madini, kuongeza ushiriki wa watanzania katika miradi ya uchimbaji wa madini pamoja na kuhamasisha matumizi ya teknolojia rafiki kwa mazingira na zinazoongeza usalama migodini.

Aidha, amewataka wananchi kutembelea banda la Tume ya Madini ili kupata elimu kuhusu huduma zinazotolewa na Tume pamoja na fursa zilizopo katika mnyororo wa thamani wa madini, ikiwemo taratibu za kushiriki biashara ya madini na kuuza madini kupitia masoko na vituo vya ununuzi wa madini.

Katika hatua nyingine, Dkt. Lekashingo amewapongeza viongozi na watumishi wa Tume ya Madini kwa kuvuka lengo la ukusanyaji wa mapato katika mwaka wa fedha 2025/2026, akisema mafanikio hayo yanadhihirisha uwajibikaji na usimamizi madhubuti wa sekta ya madini.

“Mmetuheshimisha kwa kuvuka lengo la ukusanyaji wa mapato, lakini tusibweteke. Bado tuna wajibu mkubwa wa kuhakikisha tunavuka lengo la kukusanya shilingi trilioni 1.4 katika mwaka wa fedha 2026/2027,” amesema.

Wakati huohuo, Dkt. Lekashingo ametembelea mabanda mbalimbali ya taasisi zilizo chini ya Wizara ya Madini, ikiwemo Tume ya Madini, Shirika la Madini la Taifa (STAMICO), Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST), Kituo cha Jemolojia Tanzania (TGC) na Wadau wa Madini kabla ya kutembelea mabanda ya Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), Banda la Zanzibar na Wizara ya Nishati.

Akiwa katika banda la Wizara ya Nishati, Dkt. Lekashingo ameiomba Wizara hiyo kupitia Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kuhakikisha umeme unafikishwa katika maeneo yote yenye shughuli za uchimbaji na uchenjuaji wa madini nchini ili kuongeza tija kwa wachimbaji, kuimarisha uzalishaji, kuongeza thamani ya madini na kuendeleza mchango wa sekta ya madini katika ukuaji wa uchumi na Pato la Taifa.











 



-Asema kasi ya maendeleo chini ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, amani, uchumi, afya, maji na miundombinu vimemshawishi kubadili msimamo wa kisiasa.

Na Oscar Assenga,TANGA

Baada ya zaidi ya miaka 30 ya kuwa mwanasiasa wa upinzani, aliyekuwa Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Wilaya ya Tanga, Rashid Jumbe, amefanya uamuzi mkubwa wa kisiasa kwa kujiunga na Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Jumbe, ambaye kwa muda mrefu alikuwa mmoja wa viongozi mashuhuri wa Chadema mkoani Tanga, amesema uamuzi wake umetokana na kuridhishwa na utekelezaji wa miradi ya maendeleo pamoja na juhudi za Serikali ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan katika kuimarisha amani, umoja na ustawi wa wananchi.

Akizungumza wakati wa hafla ya kumpokea ndani ya CCM iliyoongozwa na Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Tanga, Rajab Abdurhaman, Jumbe alisema hakufanya uamuzi huo kwa papara, bali baada ya kutafakari kwa kina na kujiridhisha kuhusu mwelekeo wa maendeleo ya taifa.

"Nilikuwa mpinzani kwa zaidi ya miaka 30, lakini leo nimeamua kuhitimisha safari hiyo. Kilichonishawishi zaidi ni kazi kubwa inayofanywa na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan katika kuwaletea Watanzania maendeleo na kuhakikisha amani ya nchi inalindwa," alisema.

Alieleza kuwa pia amevutiwa na utekelezaji wa falsafa ya 4R inayosisitiza maridhiano, ustahimilivu, mageuzi na kujenga upya, akisema imeongeza mshikamano na kuimarisha mazingira ya maendeleo nchini.



Akizungumzia Mkoa wa Tanga, Jumbe alisema mabadiliko yanayoonekana katika sekta mbalimbali ni ushahidi wa dhamira ya Serikali ya kuufungua mkoa huo kiuchumi.

Alitaja kuongezeka kwa shughuli katika Bandari ya Tanga, ujenzi wa bandari kavu pamoja na utekelezaji wa miradi mingine ya kimkakati kuwa miongoni mwa hatua zilizochochea ukuaji wa uchumi na kuongeza fursa za biashara.


"Nimekuwa nikipaza sauti kwa miaka mingi nikitaka Tanga ifunguliwe kiuchumi. Leo naona hilo limefanyika. Mizigo imeongezeka bandarini, bandari kavu zimejengwa na shughuli za biashara zinaendelea kukua," alisema.

Katika sekta ya afya, Jumbe alisema maboresho yaliyofanyika katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Tanga Bombo, upatikanaji wa dawa na vifaa tiba pamoja na ujenzi wa zahanati katika kata na mitaa mbalimbali vimempa imani kuwa Serikali inaendelea kuboresha huduma kwa wananchi.

Aidha, alisema upanuzi wa huduma za maji na umeme pamoja na utekelezaji wa mpango wa Bima ya Afya kwa Wote ni miongoni mwa hatua zinazoonyesha dhamira ya Serikali ya kuinua maisha ya Watanzania.

"Nilijiuliza ni hoja gani itanifanya nibaki upinzani wakati maendeleo yanaonekana wazi. Tanga ina amani, huduma zinaimarika na wananchi wanaendelea kunufaika na miradi ya maendeleo," alisema.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Tanga, Rajab Abdurhaman, alisema chama hicho kinaendelea kuimarisha umoja na mshikamano ili kuongeza uwezo wake wa kusimamia maendeleo na kuwatumikia wananchi.



Alisema tangu alipopewa dhamana ya kuongoza CCM mkoani humo, ameweka mkakati wa kuimarisha chama kupitia ushirikiano na wanachama pamoja na kuwakaribisha viongozi kutoka vyama vingine vya siasa.

Rajab alisema mkakati huo umeendelea kuzaa matunda, akieleza kuwa kujiunga kwa Rashid Jumbe ni ishara ya kuongezeka kwa imani ya baadhi ya viongozi wa upinzani kwa juhudi za maendeleo zinazotekelezwa na Serikali.

"Jumbe alikuwa mmoja wa viongozi wakubwa wa upinzani katika Wilaya ya Tanga. Tuliahidi kwamba tutamshawishi aje kushirikiana nasi katika kujenga chama na kuwaletea wananchi maendeleo, na leo tumefanikiwa," alisema.</



Na Janeth Raphael MichuziTv 

Serikali imewataka wanachama wa vyama vya ushirika nchini kuwa mstari wa mbele katika kulinda amani ya Tanzania kwa kuchagua viongozi waadilifu, kushiriki kikamilifu katika shughuli za vyama vyao na kusimamia rasilimali za ushirika kwa uwajibikaji ili kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

Wito huo umetolewa na Naibu Waziri wa Kilimo,  David Silinde (Mb), aliyemwakilisha Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Ushirika Duniani yaliyofanyika Julai 6, 2026, jijini Dodoma.

Akifunga maadhimisho hayo yaliyobeba kaulimbiu ya "Ushirika kwa Dunia Yenye Amani," Mhe. Silinde alisema ushirika una nafasi kubwa katika kujenga mshikamano wa jamii na kudumisha utulivu wa nchi, akisisitiza kuwa maendeleo ya vyama vya ushirika hayawezi kupatikana bila kuwepo kwa mazingira ya amani na utulivu.

Amesema kila mwanaushirika ana wajibu wa kuwa mlinzi wa amani kwa kuhakikisha anashiriki katika uchaguzi wa viongozi waadilifu, kushiriki vikao vya vyama vyao na kutoa mchango katika maamuzi yanayolenga kuviimarisha vyama hivyo.

"Ushirika hustawi katika mazingira ya amani, mshikamano na ushirikiano. Hivyo, kila mwanaushirika ana jukumu la kulinda tunu hiyo muhimu kwa maendeleo ya Taifa," alisema Mhe. Silinde.

Katika hatua nyingine, Naibu Waziri huyo alitoa onyo kali kwa watu wanaojihusisha na ubadhirifu wa mali za vyama vya ushirika, akisisitiza kuwa Serikali haitamvumilia mtu yeyote atakayebainika kutumia vibaya mali za wanachama au kukiuka sheria za usimamizi wa vyama vya ushirika.

Aidha, amewataka wanachama kuwa na utamaduni wa kushiriki kikamilifu katika shughuli za vyama vyao, akieleza kuwa ushiriki wa wanachama ndiyo msingi wa kujenga vyama vyenye nguvu, uwajibikaji na uwezo wa kuchangia maendeleo ya wananchi na Taifa kwa ujumla.

Kwa upande wake, Msajili na Mtendaji Mkuu wa Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania (TCDC), Dkt. Benson Ndiege, alisema sekta ya ushirika inaendelea kupiga hatua kubwa kutokana na maboresho mbalimbali yanayofanywa na Serikali, hususan matumizi ya mifumo ya kidijitali katika uendeshaji wa vyama vya ushirika.

Amesema matumizi ya teknolojia yameongeza uwazi, ufanisi, uadilifu na uwajibikaji katika usimamizi wa shughuli za ushirika, sambamba na kuhakikisha sheria, kanuni na misingi ya utawala bora inazingatiwa.

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Tanzania Federation of Cooperatives (TFC),  Tito Haule, alisema mchango wa sekta ya ushirika katika uchumi wa Taifa unaendelea kuongezeka kwa kasi, huku akibainisha kuwa mauzo ya mazao kupitia vyama vya ushirika yamefikia thamani ya shilingi trilioni nne.

Amesema mafanikio hayo yanaonesha nafasi muhimu ya ushirika katika kuwawezesha wakulima na kuchochea ukuaji wa uchumi wa nchi, huku akitoa wito kwa wanachama kuendelea kuimarisha ushirikiano na kusimamia vyama vyao kwa uwajibikaji ili kuongeza tija na manufaa kwa wanachama pamoja na Taifa.

Maadhimisho ya Siku ya Ushirika Duniani mwaka 2026 yamehitimishwa kwa msisitizo wa kuendelea kuimarisha ushirika kama chombo muhimu cha kujenga uchumi shirikishi, kulinda amani na kuharakisha maendeleo endelevu nchini.












Top News