Kuelekea Maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Wanawake, wanawake kutoka Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) wametembelea Gereza la Segerea jijini Dar es Salaam na kutoa msaada wa vifaa na mahitaji mbalimbali kwa ajili ya kuwafariji wafungwa wanawake na watoto wanaoishi gerezani hapo.

Katika ziara hiyo, wanawake hao walikabidhi mahitaji muhimu kwa uongozi wa gereza ikiwemo vyakula, mavazi, taulo za kike, maziwa ya watoto pamoja na vifaa vya usafi, ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono jitihada za kuboresha ustawi wa wafungwa wanawake na watoto waliopo gerezani.

Kwa niaba ya Mkuu wa Gereza, Mrakibu Msaidizi wa Magereza, Ngajebule Mbuguru, aliishukuru TCAA kwa msaada huo akibainisha kuwa unaleta faraja kwa wafungwa na kuwakumbusha kuwa bado ni sehemu ya jamii inayowajali.

Aliongeza kuwa vifaa na mahitaji yaliyotolewa vitasaidia kukidhi baadhi ya mahitaji muhimu ya kila siku ya wafungwa wanawake na watoto waliopo gerezani, huku Jeshi la Magereza likiendelea kutoa mafunzo ya ujuzi mbalimbali kwa wafungwa ili kuwaandaa kujitegemea pindi watakaporejea katika jamii.

Kwa niaba ya uongozi wa TCAA, Afisa Rasilimali Mkuu, Grace Kiunsi, alisema hatua hiyo ni sehemu ya utamaduni wa Mamlaka kushiriki katika shughuli za kijamii na kuendelea kuunga mkono makundi yenye uhitaji maalum katika jamii.

Alisema TCAA inaamini kuwa kuwatia moyo na kuwasaidia wanawake walioko katika mazingira mbalimbali ni sehemu ya kuchangia ujenzi wa jamii yenye mshikamano, utu na kujali.

Hatua hiyo imetajwa kuwa mchango muhimu katika kuimarisha mshikamano wa kijamii na kuendeleza jamii yenye usawa na huruma kwa wote, hususan katika kipindi hiki cha kuelekea Maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Wanawake.
Wafanyakazi wanawake wa TCAA wakiongozwa na Afisa Rasilimali Mkuu, Grace Kiunsi wakikabidhi msaada wa vifaa na mahitaji mbalimbali Mrakibu Msaidizi wa Magereza, Ngajebule Mbuguru kwa niaba ya Mkuu wa Gereza kwa ajili ya kuwafariji wafungwa wanawake na watoto wanaoishi gerezani hapo.
Mrakibu Msaidizi wa Magereza, Ngajebule Mbuguru akiishukuru Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) kwa kuwafaraji kwa wafungwa na kuwakumbusha kuwa bado ni sehemu ya jamii inayowajali.
Afisa Rasilimali Mkuu, Grace Kiunsi akizungumza kuhusu Mamlaka inavyoshiriki katika shughuli mbalimbali za kijamii na kuendelea kuunga mkono makundi yenye uhitaji maalum katika jamii.
Baadhi ya misaada iliyotolewa na TCAA katika gereza la Segerea
Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dkt. Asha-Rose Migiro, amekutana na kufanya mazungumzo na Katibu Mkuu wa Chama cha FRELIMO, (Msumbiji), Ndugu Chakil Felizardo Passadas Aboobacar, ambaye ameanza ziara rasmi ya kikazi kwa siku mbili nchini.

Katika mazungumzo hayo yaliyofanyika leo tarehe 6 Machi 2026, katika Ofisi Ndogo za Makao Makuu ya CCM, Lumumba, Dar Es Salaam, vyama hivyo viwili ambavyo vina urafiki na udugu wa kihistoria, vimekubaliana kuendelea kuimarisha uhusiano uliopo kati ya pande hizo mbili, hasa kushirikiana kiuchumi.




Katika kuelekea kilele cha maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani 2026 yakiendelea,kampuni ya Barrick nchini yenye ubia na serikali kupitiaa kampuni ya Twiga Minerals, imeendeleza dhamira yake ya kuhakikisha Wanawake wanapewa fursa sawa katika ushiriki wa mnyororo wa sekta ya madini ambapo imewawezesha wafanyakazi wake wanawake 5 kupata mafunzo uongozi kupitia programu ya Mwanamke wa Wakati Ujao (Female Future Programme) yanayotolewa na Chama cha Waajiri Tanzania (ATE) inayolenga kuboresha ufanisi wa wafanyakazi wa kike mahali pa kazi.

Programu ya Mwanamke wa Wakati ujao ambayo ilianzishwa mwaka 2015 imefikia kundi (Cohort) la 11 ikiwa inajumuisha wanawake wasomi kutoka makampuni mbalimbali, ilianzishwa Chama cha Waajiri Tanzania(ATE) kwa kushirikiana na Shirikisho la Vyama vya Waajiri nchini Norway na katika kipindi cha muda mfupi imekuwa msaada mkubwa katika kuwajengea uwezo katika utawala katika sehemu zao za kazi.

Akihojiwa kuhusu ushiriki katika progamu hiyo mmoja wa wahitimu kutoka mgodi wa Barrick North Mara, Edith Biita, alisema anajivunia kuajiriwa na kampuni kubwa kama Barrick ambayo imekuwa mstari wa mbele kuwapatia wafanyakazi wanawake nafasi za uongozi na nafasi inayomuwezesha kutoa maamuzi ambayo yeye na wafanyakazi wenzake wanawake ndani ya kampuni wanayo fursa ya kutoa mawazo yao na yamekuwa yakiheshimiwa bila kujali jinsia na umri wao.

Akiwa ni msomi wa fani ya uhandisi wa madini akifanya kazi katika kitengo cha Uchimbaji na milipuko (Drill and Blast) alisema mafunzo aliyopapata kupitia programu hiyo ni ya aina yake kwa kuwa yanawezesha kupata maarifa ya masuala mbalimbali hususani utawala kwa kuwa katika fani zote suala la utawala na uongozi lipo.

Naye Sella Mwangomole mtaalamu wa metolojia na maabara alisema mafunzo yanayotolewa na program hii yanawezesha kujiamini zaidi katika utawala na alitoa ushauri kuwa kuna haja ya kuwa na programu nyingi za aina hii ili ziwafikie wanawake wengi popote walipo nchini ili wasibaki nyuma katika utawala kwenye sekta mbalimbali.

“Ili wanawake wengi kutobaki nyuma silaha pekee ya kuwakwamua ni elimu na ninaposema elimu simaanishi kupata shahada za juu pekee bali ni kujifunza mambo mbalimbali na kupata maarifa, kuungana na kushirikiana ambapo watapata fursa ya kubadilishana uzoefu wa masuala mbalimbali,kupeana moyo na kupanga mikakati ya kutatua changamoto zinazowakabili”.Alisema Mwangomole.

Naye Noela Mataro alishukuru Barrick kupitia mgodi wa North Mara kwa kumpatia fursa ya kupata mafunzo haya ya utawala na kuongeza kuwa anavutiwa na sera ya kampuni ya kuwapatia nafasi za uongozi wanawake katika vitengo mbalimbali ambapo wanaendelea kufanya vizuri na kudhihirisha kuwa ujuzi hauna jinsia.

Mshiriki mwingine kutoka Barrick, Patricia Vullah, alisema Mpango wa kuwapatia wanawake mafunzo ya utawala ya Female Future Programme ni moja ya jukwaa la kuwanyanyua wanawake wa Tanzania na kuwafikisha kwenye nafasi za juu za uongozi na kutoa maamuzi.

Kwa upande wake Elda Mahenda alisema kupitia Programu hii alisema wanafundishwa masuala mengi hususani utawala wenye kuleta ufanisi kwa makampuni, kujiaamini na jinsi ya kushiriki na kuchangia mawazo katika vikao vya juu vya bodi za makampuni “Mtaala wa kufundishia unaotumika ni mzuri na ndani ya kipindi cha muda mfupi unaweza kumbadilisha mtu kuwa na maarifa na upeo mkubwa na kujiamini”, alisema.

Kampuni ya Barrick nchini imekuwa mstari wa mbele kutekeleza sera imara ya kukuza usawa wa kijinsia kwa kuwawezesha wanawake kushika nafasi za uongozi na kiufundi katika migodi yake ya Bulyanhulu,North Mara na Buzwagi ambao uko katika mchakato wa kufungwa pia inazingatia ushirikishwaji wa wanawake, mafunzo, na programu za ndani na nje zinazolenga kukuza vipaji vyao ili kuongeza uwakilishi katika ngazi za maamuzi.

Katika kuadhimisha Siku yaWanawake Duniani, Kampuni inatumia siku hii kama jukwaa la kutathmini na kuendeleza juhudi za wanawake kazini, kusaidia jamii zinayozunguka migodi na Kuchochea wanawake kuingia katika sekta ya madini ambayo awali ilitawaliwa na wanaume.

Juhudi hizi za uwezeshaji wanawake zinaendana na sera ya serikali ya kuongeza ushirikishwaji wa Watanzania (Local Content) na kuimarisha uwakilishi wa wanawake katika mnyororo wa sekta ya madini.





Meneja wa Kanda ya Kaskazini (TBS), Mhandisi Ismail Mwaipaja, akizungumza na waandishi wa habari mapema leo jijini Arusha kuhusu mafanikio na utekelezaji wa majukumu ya kanda hiyo

Mhandisi Mwaipaja amesema TBS Kanda ya Kaskazini imefanikiwa kuthibitisha ubora wa bidhaa za wazalishaji pamoja na wajasiriamali 492, ambapo kati yao 238 ni wajasiriamali wadogo. Hatua hiyo imechangia kwa kiasi kikubwa kukuza uchumi na kuhakikisha soko linakuwa na bidhaa bora na salama kwa watumiaji.

Aidha, ameeleza kuwa TBS inaendelea kuboresha huduma na kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma zake, ikiwa ni pamoja na mpango wa kujenga maabara mpya jijini Arusha ili kurahisisha upimaji na uthibitishaji wa ubora wa bidhaa.

Vilevile, TBS inaendelea kutoa mchango katika kuhakikisha ubora wa vifaa vinavyotumika katika miradi mikubwa ya maendeleo nchini, ikiwemo miradi ya ujenzi wa miundombinu ya michezo inayohusiana na maandalizi ya michuano ya Africa Cup of Nations (AFCON), kwa kuhakikisha vifaa vya ujenzi vinakidhi viwango vinavyotakiwa.


Na Ruth Kyelula, Manyara

Mkoa wa Manyara unatarajia kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani kimkoa tarehe 8 Machi 2026 katika Wilaya ya Simanjiro, huku Mkuu wa Mkoa huo, Mhe. Queen Sendiga, akitoa wito kwa jamii kuhakikisha haki za wanawake na wasichana zinalindwa na kuheshimiwa.

Akizungumza na waandishi wa habari Machi 3, 2026 ofisini kwake mjini Babati, Sendiga alisema maadhimisho hayo ni fursa muhimu ya kuhamasisha jamii kushiriki katika juhudi za kukuza usawa wa kijinsia, kuwawezesha wanawake kiuchumi na kuimarisha ustawi wao katika jamii.

Alisema Mkoa wa Manyara umekuwa ukikabiliwa na changamoto ya matukio ya ukatili wa kijinsia, lakini juhudi mbalimbali zimeendelea kufanyika ili kukabiliana na tatizo hilo. Alisisitiza kuwa wazazi na jamii kwa ujumla wanapaswa kuhakikisha watoto, hususan wasichana, wanapata haki zao na kulindwa dhidi ya vitendo vya ukatili.

Sendiga alieleza kuwa chimbuko la Siku ya Wanawake Duniani linatokana na harakati za wanawake wafanyakazi waliopigania haki zao kazini, jambo linaloifanya siku hiyo kuwa jukwaa la kuhimiza uwajibikaji kwa wanawake pamoja na kuwakumbusha waajiri, taasisi na serikali kuhakikisha mazingira ya kazi yanazingatia usawa wa mishahara, maslahi na fursa.

Aliongeza kuwa Tanzania imekuwa ikiadhimisha siku hiyo tangu mwaka 1997 kwa lengo la kutambua mchango wa wanawake katika maendeleo ya taifa, huku kaulimbiu ya mwaka huu ikiwa ni “Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana: Msingi Jumuishi kufikia Dira 2050.”

Mhe Mbunge wa Jimbo la Mlimba,Dkt KellenRose Rwakatare, ametembelea mabinti 300 wanaosoma katika Chuo cha Maendeleo FDC Ifakara na kuwapatia mahitaji mbalimbali muhimu kwa ajili ya kuendeleza masomo yao ya ufundi stadi.

Ziara hiyo imelenga kuwatia moyo, kuwasikiliza pamoja na kuthibitisha dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan katika kuwawezesha vijana wa kike kielimu na kiuchumi.

Akizungumza na mabinti hao, Mhe Mbunge aliwahimiza kusoma kwa bidii, kutumia vyema fursa waliyoipata na kuwa chachu ya mabadiliko katika jamii. Ziara hiyo pia ilisindikizwa na viongozi mbalimbali wa Wilaya ya Kilombero waliopongeza juhudi hizo za maendeleo




 

Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) Mkoa wa Dodoma unashiriki katika Kliniki maalum ya kutatua kero na changamoto mbalimbali za wananchi iliyoandaliwa na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, inayofanyika tarehe 3 hadi 6 Machi, 2026 katika viwanja vya Nyerere Square jijini Dodoma.

Kupitia kliniki hiyo, TBA inakutana na wateja wake ambao ni wapangaji wa nyumba zake kwa lengo la kusikiliza na kutatua changamoto pamoja na kero mbalimbali zinazojitokeza katika maeneo wanayoishi.

Aidha, kliniki hiyo imekuwa fursa kwa taasisi mbalimbali za Serikali kutoa elimu kwa wananchi pamoja na kueleza mafanikio yaliyopatikana katika utekelezaji wa majukumu yao ndani ya siku 100 za Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan tangu kuingia madarakani.

Katika kliniki hiyo, TBA kama zilivyo taasisi nyingine za Serikali imeweka banda maalum kwa ajili ya kutoa elimu kwa wananchi kuhusu majukumu yake pamoja na kueleza miradi mbalimbali iliyotekelezwa na wakala huo katika kipindi hicho.

Akitembelea mabanda ya taasisi mbalimbali katika viwanja hivyo leo Machi 5, 2026, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule, ameipongeza TBA kwa kutekeleza miradi mikubwa ya Serikali katika mkoa wa Dodoma, ikiwemo ujenzi wa Mji wa Serikali Mtumba pamoja na mradi wa ujenzi wa nyumba 3,500 za makazi ya watumishi wa umma katika eneo la Nzuguni.

Kwa upande wao, wananchi waliotembelea banda la TBA wamepongeza utekelezaji wa mradi wa nyumba za makazi katika eneo la Nzuguni, wakisema umechangia kusogeza huduma za kijamii na biashara karibu na wananchi pamoja na kuimarisha hali ya ulinzi na usalama katika eneo hilo.

 

 

Na Mwandishi Wetu, Handeni

Wanawake katika Halmashauri ya Mji Handeni wametakiwa kutumia simu janja na teknolojia ya kidijitali kwa kuwa ni nyenzo muhimu ya kukuza biashara na kujikwamua kiuchumi kupitia fursa mbalimbali zinazopatikana mtandaoni.

 Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese ameyasema hayo wakati akizindua Jukwaa la Uwezeshaji Wanawake Kiuchumi katika kongamano la wanawake lililofanyika mjini Handeni.

Amesema matumizi sahihi ya simu janja yanaweza kuwasaidia wanawake kupanua masoko ya biashara zao kupitia mitandao ya kijamii pamoja na kupata taarifa muhimu za fursa za kiuchumi zinazotolewa na serikali.

Nyamwese amesema jukwaa hilo limekuja wakati muafaka kutokana na juhudi za serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan katika kuwawezesha kiuchumi wanawake na wasichana.

“Jukwaa hili litawawezesha kupata fursa na kujadiliana namna ya kujikwamua. Mtapata mbinu mbalimbali za kuongeza thamani ya biashara zenu na namna ya kuzifikia fursa zinazotolewa na serikali ikiwamo mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na halmashauri,” amesema.

Aidha, amewasisitiza wanawake kuwa wabunifu katika biashara zao na kutumia kikamilifu teknolojia pamoja na mikopo inayotolewa na halmashauri ili kujiongezea kipato.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Handeni, Maryam Ukwaju amesema halmashauri imeandaa mkakati wa kusaidia vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu kujiunga kwenye mfumo wa ununuzi wa umma wa NeST ili viweze kunufaika na fursa ya asilimia 30 ya zabuni zinazotolewa kwa makundi hayo.

Amesema kupitia mfumo huo vikundi vitapata nafasi ya kushiriki kikamilifu katika zabuni zinazotangazwa na halmashauri na hivyo kuongeza kipato na kukuza uchumi wao.

Akizungumza kuhusu kongamano hilo, Mkurugenzi huyo amesema katika kongamano hilo wanawake walipata elimu mbalimbali ikiwamo masuala ya fedha, msaada wa kisheria, umiliki wa ardhi pamoja na masuala ya ndoa ili kuwajengea uelewa na kuwasaidia kuwa chachu ya maendeleo ya Handeni.

Aliongeza kuwa elimu hiyo pia inalenga kuwawezesha wanawake kushiriki kikamilifu katika kufikia malengo ya maendeleo ya Taifa yaliyowekwa katika Dira ya Maendeleo ya mwaka 2050.

Akisoma taarifa ya uendeshaji wa shughuli za majukwaa ya uwezeshaji wananchi kiuchumi, Mratibu wa majukwaa hayo, Carin Umwambe amesema jukwaa hilo linalenga kuwaunganisha wanawake wajasiriamali na watoa huduma katika sekta za umma na binafsi ili waweze kupata fursa mbalimbali za kiuchumi na kibiashara.

Balozi wa Switzerland nchini Tanzania, Nicole Providoli akishirikiana na viongozi mbalimbali wa Kampuni ya Sika Tanzania wakikata Utepe kuashiria usheherekeaji wa miaka 10 ya kampuni hiyo pamoja na uzinduzi wa mitambo mipya ya kisasa katika miji ya Dar es Salaam na Mwanza. 


KAMPUNI ya kimataifa ya uzalishaji wa kemikali maalum za ujenzi, Sika Tanzania, imeadhimisha miaka 10 ya uwepo wake nchini kwa kuzindua mitambo mipya ya kisasa katika miji ya Dar es Salaam na Mwanza. Hatua hiyo inalenga kuimarisha uzalishaji wa ndani, kuongeza ajira na kuchochea maendeleo endelevu katika sekta ya ujenzi.

Akizungumza katika hafla ya maadhimisho hayo, Meneja Mkuu wa kampuni hiyo, Dennis Ott, alisema uwekezaji huo unaashiria hatua mpya ya ukuaji wa viwanda na ubunifu nchini. Alieleza kuwa upanuzi wa kiwanda cha Dar es Salaam utaongeza uwezo wa uzalishaji na ufanisi wa shughuli za kampuni.

Ott aliongeza kuwa kiwanda kipya cha Mwanza kimejengwa kimkakati ili kuhudumia Kanda ya Ziwa na maeneo ya Magharibi mwa Tanzania, hatua itakayorahisisha upatikanaji wa bidhaa za ujenzi na kuimarisha usambazaji wake katika maeneo hayo.

Kwa mujibu wa kampuni hiyo, uwekezaji huo utaongeza uzalishaji wa ndani, kupunguza utegemezi wa bidhaa zinazoagizwa kutoka nje na kufungua nafasi mpya za ajira katika sekta za uzalishaji na teknolojia za ujenzi.

Katika kipindi cha miaka 10 iliyopita, Sika Tanzania imechangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya sekta ya ujenzi nchini kupitia teknolojia za kuunganisha, kuziba na kuzuia maji pamoja na suluhisho za kisasa za zege zinazotumika katika miradi mikubwa ya miundombinu.

Kupitia programu ya mafunzo ya Sika Academy, kampuni hiyo imefanikiwa kufundisha zaidi ya mafundi na wakandarasi 5,000 wa ndani, hatua iliyosaidia kuimarisha ujuzi wa wataalamu wa sekta ya ujenzi nchini.

Aidha, kampuni hiyo imeshiriki katika zaidi ya miradi 100 mikubwa ya miundombinu na biashara nchini, ikiwemo Julius Nyerere Hydropower Project, Standard Gauge Railway na Kijazi Interchange.

Wakati huo huo, Balozi wa Switzerland nchini Tanzania, Nicole Providoli, amesema Serikali ya Tanzania inaendelea kuunganisha nguvu za wadau mbalimbali kulinda mazingira na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi. Amesisitiza umuhimu wa kuendeleza sera na mikakati ya nishati safi, uhifadhi wa rasilimali za asili na matumizi ya teknolojia rafiki kwa mazingira ili kulinda ustawi wa kizazi cha sasa na kijacho.

Kwa upande wake, Meneja wa Usalama Mahali pa Kazi wa Sika Tanzania, Doto Damian, ambaye pia ni mshindi wa tuzo ya usalama mahali pa kazi, amesema kutambuliwa kwake kupitia tuzo hiyo ni motisha kubwa katika kuendelea kuhimiza utamaduni wa usalama kazini. Amesema mafanikio hayo yanatokana na juhudi za pamoja za wafanyakazi na uongozi wa kampuni katika kuhakikisha mazingira ya kazi yanakuwa salama na yenye tija.

Aidha, Damian amesema ameendelea kutoa elimu kwa mafundi na wadau wa sekta ya ujenzi kuhusu matumizi ya teknolojia ya Kiswisi katika ujenzi wa madaraja hapa nchini. Ameeleza kuwa teknolojia hiyo inasaidia kuongeza ubora, uimara na usalama wa miundombinu ya madaraja, huku akisisitiza umuhimu wa kuzingatia kanuni za usalama na matumizi sahihi ya vifaa vya kisasa katika miradi ya ujenzi.

Picha ya Pamoja ya Balozi wa Switzerland nchini Tanzania, Nicole Providoli na washindi wa tuzo mbalimbali.
Na Khadija Kalili,Kibaha
WAZIRI wa Wizara ya Ujenzi ambaye pia ni Mhe.Mbunge wa Jimbo la Mkuranga Abdallah Ulega amesema kuwa barabara ya TAMCO Mapinga itakamilika katika msimu ujao wa fedha na kuwataka wananchi waendelee kuwa wastahmilivu na adha wanayoipitia sasa.

Waziri Ulega amesema hayo katika kikao cha siku moja cha Bodi ya Barabara ya Mkoa wa Pwani(RRB/CR/01/2025/2026) kilichofanyika tarehe 4 Machi 2026 kwenye Ukumbi wa Mikutano uliopo katika jengo la Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani.

Barabara hiyo inayotoka TAMCO Kibaha hadi Mapinga ambayo pia inaunganisha Mkoa wa Pwani na Dar es Salaam kuwa ni muhimu sana iweze kukamilika katika kukuza uchumi na kurahisisha kazi za kila siku kwa jamii nzima.

Aidha amezitaja barabara zingine ambazo ziko katika mpango mkakati wa ujenzi kuwa ni Bagamoyo kwenda Mlandizi,Makofia hadi Mzenga na barabara ya Kibaha hadi Kiluvya pamoja na barabara zingine muhimu huku lengo likiwa kuunganisha Mkoa .

Waziri Ulega amesema kuwa atahakikisha barabara hizo anaziwekea fedha na zipate wakandarasi ili zianze kujengwa huku akisema atatoa kipaumbele kwa miradi mikubwa ya kimkakati yenye sura ya Kitaifa ukiwemo ujenzi wa barabara ya Kibaha ambayo kwa hatua ya awali itajengwa Kilomita 3.6 ambapo kukamilika kwake kutatoa sura nzuri na muonekano uliobora kwa Manispaa ya Kibaha ambayo ndiyo lango kwa Mikoa yote na nchi jirani.

Wakati huohuo Mbunge wa viti Maalum Kibaha Vijijini Mhe.Hawa Mchafu amesema kuwa barabara ya Kongowe - Soga inayoelekea katika Kituo cha Reli ya Mwendokasi( SGR) imekuwa ni kero na changamoto kubwa kwa wananchi wanaotumia barabara hiyo ya vumbi na kero umbali mrefu pia huwa mwiba zaidi hasa katika kipindi cha mvua.

"Tunaomba hii barabara ili iweze kukamillika ichukuliwe na TANROADS nasema hivi kwa sababu TARURA wamekua wakisuasua na kushindwa kwenda na kasi ya maendeleo ambayo wananchi wanatarajia.

Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Richard Muyungi (kulia) akizungumza jambo wakati wa kikao chake na wawakilishi wa Ubalozi wa Uingereza nchini Tanzania uliongozwa na Kiongozi wa Programu Endelevu ya Mazingira kutoka Ubalozi wa Uingereza Nchini Tanzania, Bw. Euan Davidson. Kikao hicho kilifanyika katika Ofisi ndogo ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Luthuli Jijini Dar es Salaam leo Alhamisi Machi 05, 2026.

*****************

Serikali imesema itaendelea kushirikiana na wadau wa maendeleo ili kuhakikisha vipaumbele vya Ajenda ya Mazingira na Mabadiliko ya Tabianchi vinapewa msukumo katika majukwaa ya Kitaifa na Kimataifa.

Hayo yamesemwa leo Jijini Dar es Salaam na Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Dkt. Richard Muyungi wakati wa mazungumzo baina yake naKiongozi wa Programu Endelevu ya Mazingira kutoka Ubalozi wa Uingereza nchini Tanzania, Bw. Euan Davidson.

Dkt. Muyungi amesema Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Rais Dkt. Rais Dkt, Samia Suluhu Hassan imeweka mikakati na mipango mahsusi ya kitaifa kuhusu masuala ya mazingira na tabianchi ambayo inahitaji msukumo na ushirikiano wa karibu na wadau wa maendeleo.

Ameitaja mikakati hiyo ni pamoja na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 ambapo nguzo ya tatu inaelezea kuhusu masuala ya uhifadhi wa mazingira na ustahimilivu dhidi ya mabadiliko ya tabianchi, juhudi zinazolenga kuiwezesha Tanzania kufikia nchi ya kipato cha kati ngazi ya juu ifikapo 2050.

Aidha Dkt. Muyungi amesema kipaumbele kingine kilichopewa msukumo ni pamoja na biashara ya kaboni, ambapo Serikali imeweka mazingira wezeshi kwa wadau na kwakuandaa utaratibu wa kitaifa na kimataifa kwa kuanzisha Kituo cha Taifa cha Kufuatilia Kaboni (NCMC).

“Tanzania tayari ina kanuni na miongozo ya biashara ya kaboni na Kituo cha NCMCtayari kimeanza kazi kikiwa na bodi ya wakurugenzi na kamati ya wataalamu ya uchambuzi wa miradi ya kaboni” asema Dkt. Muyungi.

Dkt. Muyungi ametaja kipaumbele kingine cha Serikali kupitia hifadhi ya mazingira ni pamoja na mkakati wa kuhamasisha jamii kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia ambapo kinara wa kampeni hiyo kitaifa na kimataifa ni Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muunganio wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Akifafanua zaidi, Dkt. Muyungi ameeleza kuwa Tanzania pia inaendelea na utekelezajina Mchango wa tatu wa kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi (NDC 3) ambao umeandaliwa kwa ajili ya kupunguza uzalishaji wa gesi joto na kujenga ustahimilivu wa mazingira.

Kwa upande wake, Kiongozi wa Programu Endelevu ya Mazingira kutoka Ubalozi wa Uingereza Nchini Tanzania, Bw. Euan Davidson amesema Ubalozi huo upo tayari kushirikiana na Ofisi ya Makamu wa Rais ili kufanikisha ajenda ya mazingira na mabadiliko ya tabianchi.

“Tupo tayari kushirikiana na Ofisi ya Makamu wa Rais katika masuala ya Uchumi wa Buluu, biashara ya kaboni, teknolojia ya nishati safi ya kupikia na ukamilishwaji wa mchango wa taifa wa kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi” amesema Bw. Davidson.
Kiongozi wa Programu Endelevu ya Mazingira kutoka Ubalozi wa Uingereza nchini Tanzania, Bw. Euan Davidson (kushoto) akizungumza jambo na Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Dkt. Richard Muyungi wakati wa mazungumzo baina yao yaliyofanyika katika Ofisi ndogo ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Luthuli Jijini Dar es Salaam leo Alhamisi Machi 05, 2026.
Mshauri wa masuala ya mazingira kutoka Ubalozi wa Uingereza Bw. Abdallah Shaha(kulia) akizungumza jambo wakati wa kikao baina ya Ubalozi huo na Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Richard Muyungi kilichofanyika katika Ofisi ndogo za Ofisi ya Makamu wa Rais, Luthuli Jijini Dar es Salaam leo Alhamisi Machi 05, 2026.
`
Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Richard Muyungi akizungumza jambo wakati kikao chake na wawakilishi wa Ubalozi wa Uingereza uliongozwa Kiongozi wa Programu Endelevu ya Mazingira kutoka Ubalozi wa Uingereza Nchini Tanzania, Bw. Euan Davidson. Kikao hicho kilifanyika katika Ofisi ndogo ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Luthuli Jijini Dar es Salaam leo Alhamisi Machi 05, 2026.


Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Richard Muyungi akiwa katika picha ya pamoja na Kiongozi wa wa Programu Endelevu ya Mazingira kutoka Ubalozi wa Uingereza nchini Tanzania, Bw. Euan Davidson muda mfupi baada ya kumalizika kwa mazunngumzo baina yao yaliyofanyika katika Ofisi ndogo za Ofisi ya Makamu wa Rais, Luthuli Jijini Dar es Salaam leo Alhamizi Machi 05, 2026.

Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Richard Muyungi akiwa katika picha ya pamoja na wawakilishi wa Ubaloziw a Uingereza nchini Tanzania muda mfupi baada ya kumalizika kwa mazunngumzo baina yao yaliyofanyika katika Ofisi ndogo za Ofisi ya Makamu wa Rais, Luthuli Jijini Dar es Salaam leo Alhamizi Machi 05, 2026.

(NA MPIGAPICHA WETU)

Top News