MKUU wa Wilaya ya Kibiti, Kanali Joseph Kolombo ameitaka Idara ya Maendeleo ya Jamii kuwasilisha majina ya vikundi vyote ambavyo havijarejesha mikopo ya asilimia 10, maarufu kama 'chechefu' vinavyokwamisha juhudi za maendeleo.

Kanali Kolombo alitoa agizo hilo Machi 17, 2026, wakati wa hafla ya utoaji wa mikopo kwa vikundi 20 kati ya 101 vilivyokidhi vigezo, ambapo jumla ya Sh milioni 266 zilitolewa kusaidia shughuli za uzalishaji.

Alisema licha ya Halmashauri kukopesha zaidi ya Sh bilioni 2 kwa vikundi mbalimbali, kiasi kilichorejeshwa hadi sasa ni takribani Sh bilioni 1 pekee, huku deni lililobaki likiwa bado kubwa.

“Fedha hizi si msaada, ni mtaji unaopaswa kurejeshwa ili kuwapa nafasi wananchi wengine kunufaika. Vikundi visivyorejesha vinakwamisha maendeleo ya wengine,” alisema Kolombo.

Aidha, alisisitiza kuwa hatua kali zitachukuliwa dhidi ya vikundi vinavyokiuka masharti ya urejeshaji, ikiwa ni pamoja na kuviita mbele ya uongozi wa wilaya ili kujua namna ya kushughulikia changamoto hiyo.

Akitoa taarifa ya utekelezaji wa mpango huo, Kaimu Mratibu wa Mikopo, Mbilima Tungaraza alisema tangu mwaka wa fedha 2016/2017, Halmashauri imetoa mikopo yenye jumla ya Sh bilioni 2 kwa vikundi 490.

Alifafanua kuwa kati ya vikundi hivyo, 178 tayari vimemaliza kurejesha mikopo yao, huku vikundi 312 vikiwa bado vinadaiwa kiasi cha zaidi ya Sh bilioni 1.

Kwa mujibu wa Tungaraza, kati ya deni hilo, takribani Sh milioni 867 ni kwa vikundi vilivyo ndani ya muda wa marejesho, wakati zaidi ya Sh milioni 384 ni kwa vikundi vilivyochelewa kurejesha mikopo hiyo.

Aliongeza kuwa Halmashauri inaendelea kuchukua hatua mbalimbali za kisheria kuhakikisha marejesho yanafanyika, ambapo katika mwaka wa fedha 2024/2025, mashauri 95 yalifunguliwa katika mahakama za Kibiti, Bungu na Mohoro, na kufanikisha ukusanyaji wa zaidi ya Sh milioni 43.

Hatua hizo, alisema, zinalenga kuhakikisha nidhamu ya urejeshaji inaimarika na mikopo hiyo inaendelea kuwasaidia wananchi wengi zaidi kujikwamua kiuchumi.



 

Na WMA – Dodoma

Watumishi wa Wakala wa Vipimo (WMA), wameitikia wito wa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania unaowataka watanzania kupitia makundi mbalimbali kupanda miti katika maeneo yao ili kuhifadhi mazingira.

Akiongoza zoezi la upandaji miti katika eneo ilipo Ofisi Kuu ya WMA Medeli jijini Dodoma, mapema leo Machi 20, 2026 Meneja Utawala na Rasilimali Watu, Charles Mavunde amewasisitiza watumishi wa Wakala hiyo nchi nzima kuzingatia maelekezo ya Serikali kwa kupanda miti na kuitunza ili kulinda mazingira.

Amesema kuwa, Mheshimiwa Rais Samia amekuwa akisisitiza mara kwa mara kuhusu upandaji miti katika maeneo mbalimbali na kwamba yeye mwenyewe ameonyesha mfano kwa kuwa kinara wa upandaji miti, hivyo WMA imeona ni vyema pia iitikie wito huo.

“Mtakumbuka kwamba, hata Mheshimiwa Dkt. Emmanuel Nchimbi, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, akimwakilisha Mhe. Rais katika maadhimisho ya siku ya upandaji miti duniani na maadhimisho ya upandaji miti kitaifa, jana Machi 19, 2026 kule Lindi aliagiza kuwa makundi mbalimbali ya watanzania waendeleze utamaduni wa kupanda miti,” ameeleza Mavunde na kuhitimisha kuwa WMA imeyachukulia kwa uzito maelekezo ya viongozi hao na itayatekeleza kikamilifu.

Viongozi na watumishi mbalimbali wa WMA Makao Makuu wameshiriki zoezi hilo la upandaji miti akiwemo Mkurugenzi wa Huduma za Biashara Phanuel Mtuki, Meneja Sehemu ya Fedha, CPA Ibrahim Mbinga, Meneja Mkoa wa Dodoma Said Ibrahim, Meneja Mawasiliano Veronica Simba na Mkuu wa Kitengo cha Mipango, Nelson Ruturagara.

Wengine walioshiriki ni watumishi kutoka Idara mbalimbali wakiwemo maafisa, maafisa usafirishaji na wasaidizi wa ofisi.

WMA ni wakala ya serikali iliyo chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara yenye jukumu kuu la kumlinda mlaji kupitia usimamizi wa matumizi sahihi ya vipimo katika sekta mbalimbali.

 
MFALME Carl XVI Gustaf wa Sweden, amemuaga aliyekuwa Balozi wa Tanzania nchini Sweden, Mhe. Mobhare Matinyi, katika hafla fupi iliyofanyika kwenye Jumba la Kifalme jijini Stockholm, leo tarehe 19 Machi, 2026.

Katika mazungumzo yao mafupi, viongozi hao walijadiliana namna ya kuendelea kuimarisha ushirikiano baina ya nchi hizi mbili katika sekta za nishati, mazingira, kilimo, utalii, miundombinu, madini na teknolojia.

Mfalme Gustaf aliipongeza Tanzania kwa kuweka utulivu nchini na kubuni mipango thabiti ya kutafuta maendeleo na kukuza uchumi wake licha ya changamoto nyingi zinazoikabili dunia nzima hivi sasa.

Balozi Matinyi alimshukuru Mfalme Gustaf kwa ushirikiano mzuri alioupata katika kipindi alichohudumu nchini Sweden ambapo Tanzania imefaidika katika sekta za nishati, kilimo, miundombinu, teknolojia na elimu ya juu.

Hii ilikuwa mara ya tatu kwa Balozi Matinyi kukutana na Mfalme Gustaf tangu awasili nchini Sweden mwezi Mei 2025. Mara ya kwanza ilikuwa wakati wa kukabidhi hati zake za utambulisho tarehe 12 Juni, 2025, na tarehe 9 Desemba, 2025, kwenye mazungumzo ya kibalozi ya mwisho wa mwaka.

Imetolewa na Ubalozi wa Tanzania, Stockholm, Sweden,
19 Machi, 2026.

Arusha, Tanzania
KAMPUNI Airtel Tanzania imeendelea kuimarisha nafasi yake kama mshirika muhimu katika mabadiliko ya uchumi na maendeleo ya kidijitali nchini, kufuatia ushiriki wake katika Mkutano wa Minority Interest Forum (MIF) 2026, ambapo kampuni hiyo iliwasilisha mafanikio yake ya kifedha, uwekezaji unaoendelea, pamoja na mchango wake kwa mapato ya Serikali.

Mkutano huo, ulioandaliwa na Office of the Treasury Registrar, uliwakutanisha viongozi wa kampuni zenye umiliki wa hisa wa Serikali kwa lengo la kujadili masuala ya utawala bora, ubunifu, na uundaji wa thamani ya muda mrefu katika mazingira ya biashara yanayobadilika kwa kasi.

Akizungumza wakati wa mkutano huo, Mkurugenzi Mtendaji wa Airtel Tanzania, Charles Kamoto, alisisitiza dhamira ya kampuni hiyo ya kuendelea kutoa thamani endelevu kupitia utawala bora wa kampuni, uwekezaji thabiti, na ushirikiano wa kimkakati.

“Airtel Tanzania itaendelea kujitolea kutoa thamani halisi kwa wanahisa huku ikichangia maendeleo ya kijamii na kiuchumi ya nchi. Safari yetu inaonesha nguvu ya ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi,” alisema.

Airtel Tanzania, ambayo Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inamiliki asilimia 49 ya hisa, ilieleza mchango wake mkubwa kiuchumi, ikibainisha kuwa kati ya mwaka 2021 hadi 2025, kampuni hiyo imelipa takribani dola za Marekani milioni 643 kama kodi na tozo mbalimbali, pamoja na dola milioni 110 kama gawio na michango maalum kwa Serikali.

Katika Siku ya Gawio ya mwaka 2025, Airtel Tanzania ilikabidhi hundi ya Shilingi bilioni 73, ikiwa miongoni mwa wachangiaji wakubwa wa gawio kwa Serikali. Kampuni hiyo pia ilitambuliwa na Tanzania Revenue Authority kama mlipakodi bora zaidi kitaifa kwa mwaka wa fedha 2023/24.

Airtel inaendelea kuwa mstari wa mbele katika kukuza ujumuishaji wa kifedha, ikiwa na zaidi ya wateja milioni 20.4, huku zaidi ya watumiaji milioni 14 wakitumia huduma za Airtel Money. Kupitia huduma kama Timiza Akiba, Kamilisha, na Afya Bima, kampuni inaendelea kupanua upatikanaji wa huduma za kifedha kwa wakulima, wajasiriamali, na jamii zisizofikiwa kwa urahisi.

Aidha, Airtel Tanzania imewekeza dola milioni 316 kati ya mwaka 2021 hadi 2025 katika kuimarisha miundombinu ya kidijitali, ikiwa na zaidi ya tovuti 3,600 za mtandao zilizo na 4G, pamoja na upanuzi wa huduma za 5G katika maeneo muhimu ya kimkakati. Kampuni pia imejenga zaidi ya kilomita 3,700 za mkongo wa mawasiliano (fibre optic) ili kuboresha mawasiliano nchini.

Kupitia ushirikiano na Universal Communications Service Access Fund, Airtel imefanikiwa kupanua huduma za mawasiliano katika maeneo ya vijijini na yasiyofikiwa kwa urahisi, kuunga mkono azma ya Serikali ya kuhakikisha upatikanaji wa mawasiliano kwa wote.

Kampuni pia inaendelea kutekeleza miradi ya kijamii, ikiwemo kuunganisha shule kwenye mtandao wa intaneti kupitia ushirikiano na UNICEF, pamoja na kuendeleza ubunifu na ujuzi wa kidijitali kwa vijana.

Wakati Tanzania ikiendelea kuelekea kwenye uchumi shindani wa kidijitali, Airtel Tanzania imeendelea kuthibitisha dhamira yake ya kuimarisha ushirikiano na taasisi za Serikali pamoja na wadau wengine, ili kuhakikisha uwekezaji endelevu, ubunifu, na uundaji wa thamani kwa wanahisa na taifa kwa ujumla.









Shauku na hamasa ya kushiriki mbio za Yas Kili International Half Marathon (21kms) imeonekana wazi miongoni mwa wakazi wa mikoa ya Kaskazini, baada ya idadi kubwa ya watu kujitokeza katika vituo vya kuchukua kits (jezi, nambari na vifaa vingine vya washiriki).

Vituo vya Moshi na Arusha vimepokea idadi kubwa ya wadau wenye shauku kubwa ya kushiriki mbio hizo huku wengi wakiwa wametimiza hatua hiyo ya awali ili kuepuka usumbufu siku ya mbio. Wakizungumza na waandishi wa habari, kwa nyakati tofauti, baadhi ya wakazi walieleza furaha yao na matarajio yao kwa mashindano hayo

Ni mara yangu ya kwanza kushiriki Yas Kili International Marathon, na nimefurahi sana. Kwa kweli, mbio hizi zina faida nyingi katika mkoa wetu kiuchumi lakini kwa washiriki kama mimi najiweka fit kiafya na mwanzo wa kufahamiana na watu mbalimbali” alisema Ester Msale, mkazi wa Moshi.

Kwa upande wake, Juma Ally ambae ni mkazi wa Arusha alisema: “Leo nimewahi hapa ili kuhakikisha nachukua kit yangu mapema tayari kwa kushiriki kilomita 21. Kwa mwaka huu kwa kweli hamasa ni kubwa sana, na nina furahi kushiriki pamoja na maelfu ya wapenzi wa mbio kutoka mikoa mbalimbali.”

Kampuni ya Mawasiliano Yas, imeendelea kuhimiza wakazi kujiandikisha mapema na kuchukua kits (jezi) zao mapema ili kuepuka usumbufu siku ya mbio. Mbio hizi hutoa fursa ya kipekee kwa washiriki kujivunia kuungana na maelfu ya wapenzi wa michezo, huku wakishirikiana kuhamasisha maisha yenye afya na jamii yenye mshikamano.

Yas Kili International Half Marathon inaendelea kuwa moja ya mashindano yanayovutia zaidi nchini, ikijumuisha washiriki wa ndani na nje ya nchi.








WANANCHI wa Kitongoji cha Shuleni, Kijiji cha Holili Vijijini wilayani Rombo mkoani Kilimanjaro, wamelalamikia athari za maji ya mvua yaliyoelekezwa kwenye makazi yao kufuatia uchimbaji wa mitaro uliofanywa na Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA). 

Wakizungumza kwa nyakati tofauti na waandishi wa habari jana, wananchi hao  wamesema hali hiyo imeanza kuleta madhara tangu kuanza kwa mvua za masika.

Akizungumza kwa niaba ya wananchi, Ibrahim Tarimo amesema mitaro hiyo imeelekeza maji moja kwa moja kwenye mashamba na makazi, hali iliyosababisha baadhi ya nyumba kuingiliwa na maji na hata ukuta wa uzio wa  nyumba ya mkazi mmoja kuanguka kufuatia mvua zinazonyesha hali ambayo inaleta hofu kubwa hasa kwa watoto wanaobaki nyumbani peke yao wakati wa mchana.

Kwa upande wake, Julius Lazaro amesema changamoto hiyo ilianza tangu mwishoni mwa mwaka 2025 baada ya TARURA kutengeneza barabara na kuelekeza mitaro kwenye makazi ya wananchi, hali inayowafanya wananchi kuishi kwa hofu hasa nyakati za usiku mvua zinaponyesha.

Amesema kuwa baada ya madhara hayo, waliwasilisha malalamiko yao kwa TARURA ambao walifika eneo la tukio na kuahidi kulifanyia kazi, lakini hadi sasa bado  hatua hazijachukuliwa.

“Barabara imetengenezwa vizuri, lakini changamoto ni haya maji yanayokuja moja kwa moja kwenye makazi yetu,” amesema.

Kwa upande wake, Medilaster Tarimo amesema maji hayo yameharibu mashamba na kuingia ndani ya nyumba yake, na kwamba anahofia madhara zaidi endapo mvua zitaendelea kunyesha bila hatua kuchukuliwa.

Mwenyekiti wa Kijiji cha Holili Vijijini, Peter Mandu alisema tayari taarifa za tatizo hilo zimefikishwa kwa TARURA pamoja na kwa mkurugenzi wa halmashauri, na kwamba mhandisi alishafika eneo hilo kujionea hali halisi. 

Ameongeza kuwa ni muhimu hatua za haraka zichukuliwe ili kuelekeza maji kwenye makorongo na kuepusha madhara zaidi.

Akizungumzia Suala hilo, Meneja wa TARURA Wilaya ya Rombo, Rickson Lema amesema tayari wamefika eneo husika na kufanya ukaguzi kwa kushirikiana na wananchi na kwamba upo mpango wa kuchepusha maji hayo, lakini unahitaji makubaliano kutoka kwa wananchi hasa wamiliki wa mashamba yatakayopitishwa mtaro mpya.

“Tulishauriana na wananchi kuhusu uwezekano wa kuelekeza maji kwenye korongo. Tunawasubiri wakubaliane kupitia serikali ya kijiji ili tuanze utekelezaji wa mradi huo,” amesema Lema.

Na: Dk. Reubeni Lumbagala

Maji ni miongoni mwa huduma muhimu ya kijamii. Maji ni huduma ambayo kila mtu anahitaji tena kila siku. Utahitaji maji kwa kuoga, kupikia, kufulia, kupigia mswaki, kunyweshea mifugo, kumwagilia maua au bustani. Mambo yanayohitaji maji ni mengi. Maji haya yanapaswa kusambazwa kutoka katika vyanzo vyake mathalani mito, maziwa na mabwawa hadi katika makazi ya watu ili yaweze kutumiwa. Wananchi wanataka maji yawafikie katika makazi yao, hiyo ndiyo kiu na hitaji lao.

Waziri wa Maji, Jumaa Aweso anatoa ushuhuda wa hali ya maji iliyokuwa hapo nyuma. "Kitendo cha wananchi wa maeneo mbalimbali nchini kukosa maji kuliifanya Wizara ya Maji kuwa ni Wizara ya kero na lawama, lakini kwa kazi kubwa alizofanya Rais Dk. Samia, leo Wizara imekuwa faraja kwa wananchi," anasema Aweso. Maneno  ya Waziri Aweso yanatokana na ukweli kuwa katika maeneo mengi nchini, wananchi walikabiliwa na shida ya maji, hivyo walikuwa na lawama nyingi kwa Wizara ya Maji kwani ndiyo yenye dhamana ya kuhakikisha huduma ya maji inawafikia wananchi kule walipo, hivyo Wizara ya Maji haikuwa na namna ya kukwepa lawama hizo.

Kutokana na utashi wa kisiasa uliopo wa serikali wa kutatua kero za wananchi ikiwemo kero ya ukosefu wa maji, serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan imechukua hatua stahili na madhubuti kuhakikisha Wizara ya Maji inakuwa faraja kwa wananchi kwa kuwafikishia huduma ya maji na hivyo maji kuchangia maendeleo ya sekta nyingine ili kwa pamoja kasi ya maendeleo iweze kuongezeka. 

Waziri Aweso anakiri Rais Dk. Samia ameleta mageuzi makubwa ya kimaendeleo kwani miradi ya maji iliyokuwa imekwama sasa inafanya kazi na maji yanatoka. Ni ukweli mtupu kuwa Rais Dk. Samia anaumizwa na shida ya wananchi kutembea umbali mrefu kwenda kutafuta maji ambayo wakati mwingine hayana uhakika wa kuyapata. Muda wa kufanya shughuli za kijamii na kiuchumi wananchi inabidi wautumie kutafuta maji  kwa matumizi mbalimbali kama ya kupikia, kufulia na kuogea.

Ndoa zilikuwa zipo njia panda. Wanandoa wanagombana kwa sababu mke amechelewa kurudi nyumbani kutoka kisimani, bombani au mtoni kuchota maji. Watoto wanachelewa kwenda shule kutokana na kutafuta maji. Rais Dk. Samia amefanya kazi kubwa kwa kuongeza bajeti ya Wizara ya Maji kutoka shilingi  bilioni 680.3 mwaka wa fedha 2021/2022 hadi shilingi trilioni 1.01 mwaka wa fedha 2025/2026. Mapinduzi haya makubwa yamefanikisha kuongezeka kasi ya usambazaji maji kwa wananchi hali inayoleta faraja badala ya lawama.

Rais Dk. Samia amefanikisha uzinduzi wa miradi ya maji kuwa endelevu badala ya miradi hiyo kutoa maji pale tu wanapokuja viongozi kukagua na kuzindua. Uendelevu wa miradi ya maji inatoa uhakika wa wananchi kupata maji safi, salama na yenye kutosheleza. Waziri Aweso anasisitiza Rais Dk. Samia kuwa kinara wa maji kwani miradi iliyokuwa imekwama tangu miaka ya 1970, sasa imekamilika na inatoa maji. Wizara ya Maji imekuwa faraja kwa wananchi kutokana na fedha za miradi kutolewa kwa wakati kugharamia miradi hiyo. Jambo la kufurahisha hapa ni kwamba, fedha nyingi za miradi ya maji ni mapato ya ndani (own sources) badala ya kutegemea misaada ya wahisani. 

Kwa mujibu wa Waziri Aweso, katika kipindi cha miaka minne ya uongozi wa Rais Dk. Samia, zaidi ya shilingi trilioni tatu zimetolewa kugharamia miradi ya maji, jambo linaloongeza kasi ya usambazaji maji kwa wananchi. Katika kuendeleza tabasamu kwa wananchi, Wizara ya Maji inatekeleza mpango mkakati wa ujenzi wa Gridi ya Taifa ya Maji ili kuhakikisha maji yanakuwa ya kuhakika kwa matumizi mbalimbali ya kimaendeleo.

Katika Wiki ya Maji iliyozinduliwa Machi 16 hadi 22, 2026, Wizara ya Maji ina kila sababu ya kutembea kifuambele kutokana na mafanikio makubwa yaliyopatikana likiwemo suala la upatikanaji wa maji kufikia asilimia 92.5 maeneo ya mijini na asilimia 85.2 maeneo ya vijijini. Kazi nzuri zimefanyika. Kwa maeneo ambayo maji hayajafika, dhamira ya serikali ni ile ile kuwafikishia wananchi wake wote maji safi, hivyo kazi ya kufikisha maji kwa wananchi wote inaendelea tena kwa kasi na viwango vikubwa.

Maoni: 0620 800 462.







Balozi wa Tanzania nchini Zimbabwe, Kamishna wa Polisi (CP) Suzan Kaganda, ametembelea ofisi za Mamlaka ya Bandari ya Tanzania (TPA) zilizopo mjini Harare na kufanya mazungumzo na Mwakilishi wa TPA nchini humo, Bi. Kulthum Boma kuhusu namna ya kuimarisha huduma na kuongeza ufanisi katika usafirishaji wa mizigo kupitia bandari za Tanzania.

Ziara ya Mheshimiwa Balozi Kaganda ni sehemu ya utekelezaji wa Sera ya Diplomasia ya Uchumi, ikiwa na lengo la kutambua na kuendeleza mchango wa TPA katika usafirishaji wa mizigo kutoka bandari za Tanzania kwenda nchi za Kusini mwa Afrika, ikiwemo Zimbabwe.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Bi. Kulthum Boma alieleza kuwa ofisi hiyo, yenye jukumu la masoko na huduma kwa wateja, imekuwa na mchango chanya katika kuongeza shehena ya mizigo inayoingia Zimbabwe kupitia bandari za Tanzania tangu kufunguliwa kwake rasmi mwaka 2023.

Kwa upande wake, Mheshimiwa Balozi Kaganda amepongeza mafanikio hayo na kusisitiza umuhimu wa ushirikiano wa karibu kati ya ofisi ya TPA na Ubalozi.

Vilevile ameshauri kuandaliwa kwa mikutano na wadau pamoja na wafanyabiashara nchini Zimbabwe ili kutumia majukwaa hayo kutoa elimu na kuongeza uelewa kuhusu matumizi ya bandari za Tanzania.

Hatua hiyo inatarajiwa kuchangia zaidi katika kukuza biashara na kuongeza pato la Taifa.






Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amewasihi Viongozi wa Dini kuendelea kuwekeza katika kufundisha maadili mema kwa kizazi cha sasa ili kuwa na Taifa zuri baadaye.

Makamu wa Rais amesema hayo wakati aliposhiriki Futari iliyoandaliwa na Jumuiya ya Maridhiano na Amani Tanzania (JMAT) iliyohusisha Viongozi wa Dini na Wadau wa Amani nchini, iliyofanyika Jijini Dar es Salaam tarehe 19 Machi 2026. Amesema ni vema kutoa kipaumbele cha pekee katika eneo la maadili kwa kuwa kuharibika kwa malezi ya sasa ni kuharibu kizazi kijacho.

Amesema kumekua na changamoto katika maadili na makuzi ya watoto, hivyo Viongozi wa Dini watakapoweka kipaumbele katika kufundisha maadili kwa waumini watakuwa wametoa mchango mkubwa kwa jamii na Taifa kwa ujumla.

Makamu wa Rais, ameipongeza Jumuiya ya Maridhiano na Amani (JMAT) kwa kazi kubwa waliyofanya ya kuimarisha mahusiano ya dini mbalimbali hapa nchini. Amesema Serikali inatambua na kuthamini kazi inayofanya Jumuiya hiyo ikiwa ni pamoja na kuelimisha wajibu wa viongozi wa dini na wajibu waumini katika kutambua nafasi zao kuleta amani nchini.

Makamu wa Rais amesema Tanzania inajivunia kuwa nchi ambayo wananchi wake wana ushirikiano bila kujali dini zao, hivyo ni muhimu kuendelea kusimamia ushirikiano huo.

Aidha, amesema ni muhimu kuimarisha mambo yote yaliyofanywa kipindi cha toba yaani Mwezi Mtukufu wa Ramadhan na kwaresma na kuyaendeleza.

Futari hiyo imehudhuriwa na Viongozi wa dini mbalimbali, Mabalozi wanaowakilisha nchi zao Tanzania, Wakuu wa Taasisi mbalimbali, Wasanii, pamoja na wadau wa amani nchini.
















Top News