
MichuziBlogV2
Most read Swahili blog on earth
Bonyeza play kuangalia Michuzi TV LiVE
BONYEZA PLAY KUANGALIA AZAM TV LIVE
BONYEZA KUANGALIA CHANNEL TEN LIVE

Na Mwandishi Wetu
KAMPUNI ya Kitanzania ya Ngoteya Wild, inayoongozwa na muandaaji wa makala zenye maudhui ya uhifadhi na wanyamapori @Hans_Cosmas_Ngoteya, imetangaza kuwa filamu yao mpya ya Sentinels of Engaruka ambayo wamefanya kwa kushirikiana na African people and wildlife itaoneshwa rasmi kupitia YouTube channel yao Juni 21, 2026.
Filamu hiyo imechukua zaidi ya miaka mitatu kuandaliwa, ikihusisha utafiti wa kina, upigaji picha wa mazingira ya asili na simulizi inayoonesha uhusiano wa kipekee kati ya jamii ya Kimasai, twiga na mazingira ya Engaruka mkoani Arusha.
Toleo la Kiswahili la filamu hiyo limesimuliwa na mtangazaji maarufu Meena Ally, ambaye sauti yake itaongeza mguso wa kipekee katika kuifikisha hadithi hiyo kwa watazamaji wa Tanzania na Afrika Mashariki.
Kwa mujibu wa Hans Ngoteya, filamu hiyo inalenga kuhamasisha uhifadhi wa maliasili, kuonesha utajiri wa urithi wa Tanzania na kuifikisha hadithi ya Engaruka kwa hadhira ya kimataifa kupitia jukwaa la YouTube.
Sentinels of Engaruka ni moja ya miradi mikubwa ya filamu za uhifadhi iliyotayarishwa nchini Tanzania, ikiwa na lengo la kuonesha namna jamii na wanyamapori wanavyoweza kuishi kwa maelewano huku wakilinda mazingira kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.
Tume ya Utumishi wa Umma inatarajia kufanya Mkutano wake Na. 4 wa mwaka wa fedha 2025/2026 kuanzia tarehe 15 Juni hadi 3 Julai 2026 jijini Mwanza, ambapo itajadili na kutoa maamuzi kuhusu rufaa na malalamiko mbalimbali yaliyowasilishwa na watumishi wa umma.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma tarehe 10 Juni 2026, Kaimu Katibu wa Tume ya Utumishi wa Umma, Bw. John C. Mbisso, amesema kuwa kupitia mkutano huo, Tume itatoa fursa kwa warufani na warufaniwa walioomba kufika mbele ya Tume ili kutoa ufafanuzi wa ziada kuhusu hoja zilizowasilishwa katika rufaa zao.
Bw. Mbisso amesema hatua hiyo inatekelezwa kwa mujibu wa Kanuni ya 62(1) ya Kanuni za Utumishi wa Umma za mwaka 2022, aidha Tume itapitia taarifa mbalimbali za utekelezaji wa majukumu yake katika kipindi cha robo ya tatu ya mwaka wa fedha 2025/2026.
Pamoja na shughuli za mkutano, amesema Tume itafanya ziara katika baadhi ya taasisi za serikali zilizopo jijini Mwanza kwa lengo la kutoa elimu kwa waajiri, mamlaka za ajira na mamlaka za nidhamu kuhusu umuhimu wa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu katika usimamizi wa rasilimali watu.
Vilevile ameeleza kuwa Tume itatoa elimu kwa watumishi wa umma katika taasisi hizo kuhusu haki na wajibu wao katika utekelezaji wa majukumu ya utumishi wa umma Sambamba na hilo, itapokea na kushughulikia malalamiko ya watumishi wa umma ambao hawakuridhika na maamuzi yaliyotolewa na waajiri, mamlaka za ajira au mamlaka za nidhamu.
Kwa mujibu wa Kifungu cha 12(1)(d) kikisomwa pamoja na Kifungu cha 27(1)(b) cha Sheria ya Utumishi wa Umma, Sura ya 298, Marejeo ya Mwaka 2023, Tume ya Utumishi wa Umma imepewa mamlaka ya kupokea na kushughulikia rufaa na malalamiko ya watumishi wa umma wasiokubaliana na maamuzi yaliyotolewa na waajiri, mamlaka za ajira na mamlaka za nidhamu katika utumishi wa umma.
Na Karama Kenyunko Michuzi Tv
KAMPUNI za Singapore zimeendelea kuimarisha uwekezaji wake nchini Tanzania huku kampuni ya Wilmar Rice iliyopo Morogoro ikitajwa kuwa kiwanda kikubwa zaidi cha kusindika mpunga na kuzalisha mchele si Tanzania pekee wala Afrika Mashariki, bali katika bara lote la Afrika.
Akizungumza katika Jukwaa la Biashara la Tanzania na Singapore, Juni 9, 2026 Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo amesema uwepo wa wawekezaji wa Singapore nchini unaonyesha namna ushirikiano wa kiuchumi kati ya mataifa hayo mawili unavyoendelea kukua.
"Wilmar Rice Morogoro ni kiwanda kikubwa zaidi cha kusindika mpunga na kuzalisha mchele si Tanzania pekee, si Afrika Mashariki pekee, bali kikubwa zaidi Afrika, na tunajivunia sana kampuni hii iliyopo Morogoro," amesema.
Profesa Mkumbo amesema pamoja na Wilmar Rice, kampuni ya Norman Gohines imekuwa mwekezaji muhimu Zanzibar kwa zaidi ya miaka 100 ikijikita katika uzalishaji wa viungo na shughuli za mashamba ya viungo.
Amesema kampuni hizo ni sehemu ya uwekezaji wa Singapore nchini Tanzania, huku kampuni nyingine nyingi kutoka taifa hilo zikiendelea kufanya shughuli zake nchini.
Profesa Mkumbo amesema Singapore imepitia safari ya maendeleo inayovutia dunia, ikitoka kuwa nchi ndogo yenye kipato cha chini na pato la mtu mmoja mmoja la dola 565 hadi kufikia zaidi ya dola 100,000 kwa sasa.
Amesema mafanikio hayo yameifanya Singapore kuwa na sauti muhimu katika uchumi, diplomasia na siasa za dunia.
Kwa mujibu wa Profesa Mkumbo, kampuni za Singapore ni miongoni mwa wawekezaji wakubwa duniani zikiwa zimewekeza takribani dola trilioni 1.5 katika maeneo mbalimbali duniani, hasa Asia, huku uwekezaji wake barani Afrika ukifikia kati ya dola bilioni 26 na 32 kupitia kampuni takribani 100 zinazofanya shughuli katika nchi 40.
Amesema ziara ya Rais wa Singapore, Tharman Shanmugaratnam, nchini Tanzania itasaidia kupeleka ushirikiano wa kiuchumi kati ya nchi hizo mbili katika hatua nyingine.
Profesa Mkumbo amesema mwelekeo wa kiuchumi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ni kuimarisha ushirikiano wa kimataifa kwa kuvutia biashara na uwekezaji.
"Ametuelekeza tushirikiane na dunia nzima, tusiende kutafuta misaada bali kutafuta washirika wa biashara na uwekezaji," ameisema.
Ameongeza kuwa historia ya maendeleo ya Singapore inatoa mafunzo muhimu ambayo Tanzania inaweza kujifunza na kuyatumia kwa kuzingatia mazingira yake katika safari ya maendeleo.
Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi, ameieleza Jumuiya ya Kimataifa hatua kubwa zinazochukuliwa na Serikali ya Tanzania katika kulinda na kuendeleza haki za watu wenye ulemavu, wakati aliposhiriki Mkutano wa 19 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu (COSP19) unaofanyika katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, Jijini New York, Marekani.
Mhe. Mahundi, ambaye amemuwakilisha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu–Sera, Bunge na Uratibu na Wenye Ulemavu, Mhe. Profesa Palamagamba John Kabudi, amesema Tanzania imeendelea kuimarisha mifumo ya kisheria, kisera na kiutendaji ili kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapata haki, fursa na huduma stahiki kama wananchi wengine.
Akiwasilisha taarifa ya nchi, Mhe. Mahundi amesema Tanzania imepiga hatua kubwa kupitia Sheria ya Watu Wenye Ulemavu Na. 9 ya mwaka 2010 kwa Tanzania Bara pamoja na Sheria Na.8 ya mwaka 2022 ya Zanzibar, ambazo zimeweka msingi imara wa kulinda haki na ustawi wa watu wenye ulemavu.
“Masuala ya ulemavu yamejumuishwa katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 na mipango mbalimbali ya maendeleo ili kuhakikisha hakuna anayebaki nyuma katika safari ya maendeleo ya taifa na kusema kuwa Serikali imeendelea kupanua upatikanaji wa elimu jumuishi, huduma za afya, huduma za urekebishaji na tiba, teknolojia saidizi, programu za uwezeshaji kiuchumi pamoja na huduma za hifadhi ya jamii kwa watu wenye ulemavu” @maryprisca_mahundi.
Aidha Mhe. Mahundi amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa uongozi wake madhubuti na dhamira ya dhati ya kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapata huduma bora na fursa zinazowawezesha kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya nchi.
Mkutano huo wa 19 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu umebeba kaulimbiu inayosema “CRPD at 20: Celebrating and Consolidating Achievements and Shaping the Next Phase of Implementation in a Changing World,” ukilenga kutathmini mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha miaka 20 tangu kuanzishwa kwa mkataba huo na kuweka mikakati.
.jpeg)
.jpeg)