Na Mwandishi Wetu, Berlin, Ujerumani.
MKURUGENZI wa Mauzo wa Turaco Collection Tanzania, Florenso Kirambata akiziwakilisha hotel zao katika maonesho ya ITB- Berlin anasema kwamba, maonesho hayo ni eneo jema kabisa la kujitangaza kubadilishana uzoefu hasa katika dunia ambayo walaji (watumiaji wa huduma) wamekuwa wakibadilika kutokana na mazingira yanayotokea duniani.

Florenso amebainisha kuwa, Turaco Collection kwa upande wa Dar es Salaam wana Element By Westin Marriott na Delta By Marriott na kwa upande wa utalii wa kaskazini pamoja na bidhaa mbalimbali za utalii pia wana; Turaco Ngorongoro Valley Lodge Tribute portfolio under Marriott International na Turaco Manyara View Lodge Tribute portfolio under Marriott International na kwa Zanzibar wana Turaco Nungwi Beach Reasort Tribute portfolio under Marriott International na Turaco Spice Tree Stone Town Tribute portfolio under Marriott International na Beyt Aly Salaam-By Turaco

Katika jukwaa hili linalokutanisha wadau wa sekta ya utalii kutoka kila pembe ya dunia kwa lengo la kukuza ushirikiano, ubunifu na uwekezaji endelevu.

Katika hafla hii, napenda kusisitiza kuwa Serikali ya Tanzania imeendelea kukuza mazingira rafiki ya biashara na uwekezaji, huku ikilenga kurahisisha michakato ya kiutawala, kuimarisha mifumo ya udhibiti, na kutoa motisha zinazovutia wawekezaji wa ndani na nje ya nchi.

Hatua hizi ni sehemu ya mkakati mpana wa kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha utalii wa kimataifa chenye ushindani na ubora wa hali ya juu.

Tanzania imefungua milango kwa fursa mbalimbali za biashara na uwekezaji, tayari ikiwakaribisha wadau kushirikiana katika maono ya kukuza uchumi endelevu na ustawi wa muda mrefu katika sekta ya utalii. Turaco Collection tunaamini kuwa ushirikiano kati ya sekta binafsi na Serikali ni nguzo muhimu katika kufanikisha malengo haya.

Maonesho haya ni fursa adhimu ya kubadilishana uzoefu, kuhamasisha ushirikiano wa kimkakati, na kuweka misingi ya miradi mipya itakayoboresha miundombinu, huduma, na ubora wa uzoefu wa watalii. Kupitia jukwaa hili, tunaendelea kuitangaza Tanzania kama kivutio cha kipekee chenye utajiri wa mbuga Za wanyama,Mlima Kilimajaro,utamaduni, historia, fukwe za kuvutia na huduma bora za ukarimu.

Aidha, nawapongeza Bodi ya utalii kwa kuendeleza utamaduni wa kufanya maonesho ya utalii na uwekezaji katika medani za kimataifa.

Jitihada hizi zinaimarisha taswira ya nchi yetu, kuongeza mtiririko wa watalii, na kufungua milango mipya ya masoko duniani.

Turaco Collection tunaendelea kujizatiti kutoa huduma za viwango vya kimataifa, tukizingatia ubora, ubunifu na uzoefu wa kipekee kwa wageni wetu. Tunaamini kuwa kwa pamoja, tutaweza kuifanya Tanzania na Afrika Mashariki kwa ujumla kuwa kitovu cha utalii endelevu na wenye tija kwa kizazi cha sasa na kijacho.









Na Khadija Kalili, Kibaha
MWENYEKITI wa Baraza la Wafanyakazi Mkoa wa Pwani ambaye pia ni Katibu Tawala wa Mkoa huo, Pili Mnyema, amewataka wajumbe wa baraza hilo kujadili ajenda zenye tija kwa wananchi pamoja na kufuata sheria, kanuni na taratibu za utumishi wa umma.

Mnyema ameyasema hayo leo, Machi 3, 2026, wakati wa ufunguzi wa kikao cha Baraza la Wafanyakazi Mkoa wa Pwani kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano uliopo Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Kibaha.

Aidha, amesisitiza uwajibikaji, kufanya kazi kwa nidhamu na uadilifu, pamoja na kuhimiza ushirikiano ili kutoa huduma bora kwa wananchi.

“Niwapongeze kwa mafanikio yaliyofikiwa, kwani Mkoa wa Pwani unaongoza katika mambo mengi yaliyoiwezesha kuwa kinara katika sekta mbalimbali. Hivyo, niwaombe tuendelee kushirikiana ili kuendeleza mafanikio hayo na kuufanya Mkoa wetu kuwa kinara katika kila sekta,” amesema Mnyema.

Katika hatua nyingine, amewataka wajumbe wa baraza hilo kuipa kipaumbele ajenda ya uwekezaji kwa kufanya kazi kwa ushirikiano, akieleza kuwa Mkoa wa Pwani ni mkoa wa kimkakati katika uwekezaji wa viwanda.

Aidha, kikao hicho kilipata fursa ya kupokea taarifa ya utekelezaji wa mpango wa bajeti wa mwaka 2025/2026, pamoja na kupokea na kupitisha rasimu yexa mpango wa bajeti ya mwaka 2026/2027. Vilevile, kilifanya uchaguzi wa Katibu na Katibu Msaidizi, ambapo Ramadhani Mwaiganju amechaguliwa kuwa Katibu, huku Mwajuma Mohamed amechaguliwa kuwa Katibu Msaidizi.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mhe. Wanu Hafidh Ameir, ameutaka uongozi wa Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Mzenga, kilichopo Kata ya Mzenga, Wilaya ya Kisarawe, kuhakikisha kinatoa mafunzo katika fani zinazoendana na shughuli za kiuchumi za eneo hilo.

Mhe. Wanu ametoa agizo hilo Machi 03, 2026, wilayani Kisarawe wakati wa ziara ya ufuatiliaji na ukaguzi wa miradi inayotekelezwa na Wizara katika wilaya hiyo.

Amewataka viongozi wa wilaya na wananchi wa eneo hilo kuona umuhimu wa mafunzo ya ujuzi na hivyo kuhamasisha vijana kujiunga na chuo hicho ili kupata ujuzi utakaowawezesha kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi.

Amesema chuo hicho, pamoja na vyuo vingine vya maendeleo ya wananchi, vinapaswa kuzingatia mahitaji halisi ya kiujuzi ili vijana waweze kujiunga kwa wingi.

“Mmesema hapa mnazalisha zao la korosho, ufuta na mihogo; kwa nini sasa msianzishe kozi ya kusindika mazao hayo? Hii itawamasisha vijana kujiunga na chuo kwa kuwa wanasoma kile wanachofanyia kazi,” amesema Mhe. Wanu.

Aidha, ameutaka uongozi wa chuo hicho kusimamia ipasavyo mifumo ya usimamizi wa watumishi ili kuimarisha uwajibikaji.

Akiwa wilayani humo, Mhe. Wanu pia amekagua ujenzi wa VETA Kisarawe na kusema kuwa Serikali inaendelea kujipanga kupata rasilimali fedha kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa chuo hicho ili malengo ya kutoa ujuzi kwa wananchi yafikiwe.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe, Mhe. Petro Magoti, amemuhakikishia Naibu Waziri Wanu ushirikiano katika kusimamia utekelezaji wa maagizo aliyoyatoa, ikiwemo kuhakikisha huduma za umeme na maji zinafika katika eneo la chuo ili kurahisisha hatua inayofuata ya ujenzi.








Na Mwandishi Wetu, Michuzi TV

Tanzania imeungana na mataifa mengine duniani kuadhimisha Siku ya Wanyamapori Duniani, siku maalum inayotambua mchango wa wanyamapori katika maendeleo ya kijamii, kiuchumi na kimazingira.

Akizungumzia maadhimisho hayo.

Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Utalii Tanzania, Ephraim Mafuru, amesema kuwa, kwa Tanzania wanyamapori si urithi wa asili pekee bali ni sehemu ya utambulisho wa taifa.

“Wanyamapori ni uti wa mgongo wa sekta yetu ya utalii. Ni chanzo cha ajira na kipato kwa maelfu ya wananchi. Ni fahari inayolitangaza taifa letu kimataifa,” amesema Mafuru.

Ameongeza kuwa kupitia rasilimali hizo, Tanzania imeendelea kuwa kivutio kinachoongoza duniani, kikivutia wageni kutoka pande zote za dunia kufurahia vivutio vya asili vilivyopo nchini.

Mafuru amesisitiza kuwa Bodi ya Utalii Tanzania itaendelea kuhamasisha na kukuza utalii endelevu unaolinda mazingira, unaoheshimu bioanuwai, na kuhakikisha wanyamapori wanahifadhiwa kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Maadhimisho ya mwaka huu yameongozwa na kaulimbiu isemayo, “Medicinal and Aromatic Plants: Conserving Health, Heritage and Livelihoods” (Mimea Tiba na Harufu: Kuhifadhi Afya, Urithi na Maisha), inayotukumbusha kuwa utajiri wa bioanuwai ya Tanzania si uzuri wa asili pekee, bali ni chanzo cha afya, maarifa ya jadi, ajira na ustawi wa jamii.

Kaulimbiu hiyo inaweka msisitizo katika umuhimu wa kulinda mimea tiba na rasilimali nyingine za asili kama sehemu ya mkakati mpana wa uhifadhi unaounganisha mazingira, urithi wa kitamaduni na maendeleo endelevu ya taifa.


Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Algeria, Mhe. Iman Njalikai, alikutana na kufanya mazungumzo na Rais wa Chama cha Kamati za Kitaifa za Olimpiki za Afrika (ANOCA), Bwa. Mustapha Berraf, tarehe 01 Machi, 2026, katika Ofisi za Michezo ya Vijana Afrika, jijini Algiers.

Kupitia mazungumzo hayo, wawili hao walijadili kuhusu namna ya kuimarisha ushirikiano kwenye masuala ya olimpiki. Kadhalika, waliangazia namna ya kuimarisha ushirikiano wa michezo kwa ujumla kati ya Tanzania na Algeria kupitia Wizara za Michezo za nchi hizo mbili.

Viongozi hao, walisisitiza kwamba kukamilisha na kusaini Hati ya Makubaliano (MoU) kwenye eneo la michezo, kutaimarisha ushirikiano huo. Mhe. Balozi Njalikai alisisitiza umuhimu wa kutoa kipaumbele kwenye eneo la mafunzo sambamba na kuandaa programu maalumu za mafunzo ya olimpiki kwa ajili ya vijana ili kuwajengea uwezo wa kushiriki na kufanya vizuri katika mashindano mbalimbali ya kimataifa.

Kwa upande wake Bw. Berraf alionesha utayari wa kutoa kipaumbele maalumu kwa Tanzania kwenye eneo la mafunzo na kuahidi pia kuchagiza ukamilishwaji wa MoU kwenye eneo la michezo kati ya Tanzania na Algeria.

Mhe. Balozi Njalikai, alihitimisha mazungumzo yake kwa kumshukuru Bw. Berraf kwa kuonesha nia thabiti ya kuimarisha ushirikiano pamoja na juhudi anazofanya za kukuza vipaji vya vijana wa kitanzania kimichezo.




Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, Profesa Riziki Shemdoe ameziagiza halmashauri zote kwenye mikoa ya Geita, Tabora na Iringa kuendelea kutenga kiasi cha sh 1,000 kwenye bajeti zao kwa kila mtoto wa chini ya miaka mitano ili kuboresha miradi ya lishe katika halmashauri hizo.

Ametoa maagizo hayo wakati wa uzinduzi wa Mradi wa Kuimarisha Huduma za Lishe katika mikoa ya Geita, Iringa na Tabora ili kusaidia kupunguza changamoto za udumavu, ukondefu na utapiamulo wa watoto.

Profesa Shemdoe ameitaka mikoa ya Geita, Iringa na Tabora kuimarisha ufuatiliaji wa mradi jumuishi wa lishe na shughuli zote zinazotekelezwa katika jamii kwa ajili ya kukabiliana na matatizo ya lishe

Mradi wa Kuimarisha Huduma za Lishe  unatekelezwa chini ya ufadhili wa taasisi ya BWP ya nchini Uingereza kwa thamani ya dola za kimarekani milioni 2 malengo makuu yakiwa ni kuimarisha lishe na maendeleo ya watoto.

Halmashuri zote zimetakiwa kuhakikisha zinatoa takwimu sahihi na kwa wakati ili kuzingatia utoaji huduma sahihi kwa kuzingatia ushahidi unaotokana na takwimu.

Naibu Katibu Mkuu wa TAMISEMI, Profesa Tumaini Nagu amesema kuwa kupitia  mradi huu serikali itaongeza kasi ya ufuatiliaji wa huduma bora za malezi na makuzi ya awali ya mtoto hususani katika vituo ya kulelea watoto mchana,

Mkurugenzi Msaidizi wa Huduma za Lishe Ofisi ya Waziri Mkuu TAMISEMI, Luitfrid Nnally amesema kuwa pamoja na nchi kuwa na kiwango kikubwa cha vyakula lakini bado watoto wanapata utapiamlo katika mikoa hii mitatatu kutokana na kukosa matunzo kutokana na shughuli nyingi za wazazi hususani kilimo

Mwakilishi wa taasisi ya BWP, Dr Taye Balcha alisisitiza kuwa mradi huo umezingatia tathimini ya serikali na hivo na kutambua kuwa wahanga wakubwa wa udumavu ni watoto.

Mkuu wa mkoa wa Geita, Martine Shigella aliahidi kuwa mkoa wa Geita kwa kushirikiana na mikoa inayonufaika na mradi huo watatumia fursa hiyo kupunguza kiwango cha lishe kilichopo.






 

 Mbunge wa Jimbo la Bagamoyo, Mhe. Subira Mgalu leo Machi 03, 2026 amekabidhi magari mapya kwa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Wilaya ya Bagamoyo mkoani Pwani kwa lengo la kuimarisha huduma kwa wateja na kuongeza ufanisi wa utendaji kazi katika kuwahudumia Wateja wilayani Bagamoyo.

Akizungumza katika hafla ya makabidhiano iliyofanyika Ofisi ya TANESCO Bagamoyo, Mhe. Mgalu amesema kuwa hatua hiyo ni sehemu ya jitihada za Serikali kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya umeme kwa wakati, kwa ubora na kwa uhakika zaidi.

“Magari haya yatawezesha mafundi na wahandisi wa TANESCO kuwafikia wananchi kwa haraka pale panapotokea hitilafu au changamoto za umeme. Tunataka kuona muda wa kushughulikia matatizo unapungua na huduma inaboreshwa,” amesema Mhe. Mgalu.

Amesisitiza kuwa, hivi sasa TANESCO imeimarika katika utoaji wa huduma ikiwa ni pamoja na kutoka katika kutengeneza hasara na linajiendesha bila kupata ruzuku kutoka Serikalini.

Aidha, amesema baada ya kukamilika bwawa la Julius Nyerere linalozalisha megawati 2115 na kupelekea Nchi kuwa na uwezo wa takribani wa megawati 4,000 huku mahitaji yakiwa takribani megawati 2,000 hivyo kuitaka TANESCO kuongeza kasi ya kuwaunganishia wateja.

Mkurugenzi wa TANESCO Kanda ya Mashariki,Mha. Kenneth Boymanda amesema  TANESCO inatekeleza miradi mingi ya maendeleo Wilaya ya Bagamoyo ikiwemo ya umeme Vijijini hivyo upatikanaji wa magari hayo kutarahisisha utekelezaji wa miradi hiyo.

“Bagamoyo tunao mpango mkubwa wa kuhakikisha kila nyumba inafikishiwa nishati ya  umeme nak ama Nchi mpaka mwaka 2030 kuunganisha nyumba milioni nane na laki tatu na nyumba Milioni Moja na Laki Saba kwa mwaka”, amesema Mha. Boymanda

Ameongeza kuwa, majukumu hayo yanahitaji uwepo wa vitendea kazi na kusisitiza kuwa TANESCO itafanya kazi usiku na mchana ili kuhakikisha malengo yaliyowekwa na Serikali kupitia mpango wa mission 300.

Serikali imeendelea kuweka mkazo katika kuboresha miundombinu ya umemme kama msingi wa maendeleo ya viwanda, biashara na ustawi wa jamii.

 Hatua ya TANESCO kununua magari hayo ni sehemu ya juhudi za kuimarisha huduma kwa wateja  na kuongeza ubora wa huduma kwa wananchi.


Serikali imesema itaendelea kuratibu na kuimarisha Sera, Sheria na Miongozo inayosimamia programu za Mafunzo ya Uanagenzi na kuhamasisha sekta binafsi kushiriki kikamilifu katika kutoa nafasi za mafunzo kwa vitendo kwa wanagenzi nchini.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Mkuu Kazi, Ajira na Mahusiano Deus Sangu amesema hayo  leo Machi 03,2026 katika chuo cha ufundi stadi Daon Bosco jijini Dodoma wakati akifungua  Awamu ya Nane ya Mafunzo ya Stadi za Kazi kwa Njia ya Uanagenzi kwa Vijana 5,746 waliodahiliwa katika Vyuo 46 nchini kwa mwaka 2025/26 ambapo utekelezaji wa programu umewezesha jumla ya wanufaika 93,495 hadi kufikia Februari, 2026.

Waziri Sangu amesema mafunzo hayo yanachangia kwa kiasi kikubwa katika kuwapa vijana uzoefu wa kazi kwa nadharia na vitendo, kupunguza pengo la ujuzi kati ya mafunzo ya kitaaluma na mahitaji ya waajiri na kuongezeka kwa ajira kwa vijana kuajiriwa au kujiajiri.

“Hii ni dhamira ya dhati ya Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mhe.Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kujenga nguvukazi yenye ushindani na tija kwa maendeleo endelevu ya Taifa.” amesema.

Aidha, amesisitiza kuwa kuelekea Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Tanzania inahitaji nguvukazi yenye ujuzi, weledi na uwezo wa kutumia teknolojia ili kuhimili ushindani wa kikanda na kimataifa, huku Serikali ikiendelea kuboresha sera, sheria na mifumo ya mafunzo kuongeza fursa za ajira kwa vijana.

Awali akitoa salamu za wananchi wa Dodoma, Mkuu wa Mkoa huo Rosemary Senyamule ameipongeza serikali kwa kuendelea kutenga bajeti maalum kwa ajili ya mafunzo ya uanagenzi hatua ambayo inaonyesha wazi kuwa serikali inawekeza katika rasilimali muhimu za taifa hususani Vijana.

Kwa upande wake Naibu Katibu, Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Ajira na Mahusiano Zuhura Yunus amesema Serikali kupitia Ofisi hiyo, inatekeleza Mafunzo ya Uanagenzi kupitia Programu ya Taifa ya Kukuza Ujuzi Nchini kuanzia mwaka 2016/17 na dhumuni la programu hiyo ni kukuza ujuzi wa nguvukazi iliyopo katika soko la ajira ili kuongeza tija kwenye uzalishaji wa bidhaa na utoaji wa huduma.

Naye, Mkuu wa Chuo cha Don Bosco Dodoma, Mhandisi Dkt. Justine Mulebya, ameshukuru Serikali kwa kukipatia chuo hicho wanafunzi 650 na ameiomba kuwawezesha vifaa wahitimu wa mafunzo ya uanagenzi ili kuwawezesha kujiajiri na kuajiri vijana wengine wakihitimu mafunzo yao.






Naibu Waziri wa Kilimo Mhe David Silinde amesema kuwa Serikali imeweka dhamira ya kuleta mabadiliko katika sekta ya kilimo ili kupunguza umaskini na kuongeza ajira hasa kwa vijana na wanawake na kufikia asilimia 10 ya ukuaji wa kilimo ifikapo mwaka 2030.


Mhe Silinde ameyasema hayo leo Jijini Dodoma Machi 3,2026 wakati akifungua Mkutano wa nne wa Kitaifa wa Kilimo ikolojia hai, akimuwakilisha Waziri wa Kilimo Mhe Daniel Chongolo. 

Ambapo amesema Serikali imechukua hatua za kuleta mabadiliko hayo katika sekta ya kilimo ikiwa ni pamoja na kuongeza bajeti ya Wizara kufikia trilioni 1.24 kwa 2025/2026.

"Ndugu Washiriki, nipende kuwajulisha kwamba Serikali imedhamiria kwa dhati kabisa kuleta mabadiliko makubwa katika sekta ya Kilimo ili kuchangia katika kupunguza umaskini, kuongeza ajira hususani kwa vijana na wanawake na kufikia asilimia 10 ya ukuaji wa kilimo ifikapo mwaka 2030. Katika jitihada za kuleta mabadiliko hayo, Serikali imechukua hatua mahsusi katika sekta ya kilimo ikiwa ni pamoja kuongeza bajeti ya kilimo kufikia trilioni 1.24 mwaka 2025/2026".

Aidha ameeleza kuwa Mkutano huu uliohudhuriwa na wadau kutoka ndani na nje ya Tanzania, unalenga kutafakari kwa kina namna ya kuendeleza jitihada mbalimbali za Kilimo Ikolojia Hai ikiwemo utekelezaji wa Mkakati wa Kilimo Ikolojia Hai wa 2023-2030 lengo ikiwa ni kuhakikisha kuwa viashiria vya mipango ya maendeleo ikiwemo Mpango Kabambe wa Kilimo (Agriculture Master Plan), Mpango Jumuishi wa Maendeleo ya Kilimo Afrika (CAADP), Dira ya Maendeleo na Malengo Endelevu ya Maendeleo (SDGs) vinatekelezwa kufikia utoshelevu wa chakula nchini kwa kuzingatia lishe bora na utunzaji wa mazingira.

Na kuongeza kuwa katika kutekeleza maazimio ya mkutano wa Tatu wa Kilimo Ikolojia Hai uliofanyika mwaka 2023, Serikali imetenga fedha kwenye bajeti ya Wizara ya mwaka 2025/26 kwa ajili ya utekelezaji wa Mkakati wa vyuo kuanza kufundisha Kilimo Ikolojia, mfano Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine (SUA). na Wizara kufanya jitihada mbalimbali za kutunza mbegu za asili kupitia Taasisi ya Utafiti wa Kilimo kwa kukusanya, kusafisha na kuhifadhi jumla ya mbegu za asili 770 za mazao ya ulezi, mpunga, mtama, uwele, migomba, maharage na papai,  

Ambapo Wizara kupitia TOSCI tayari imekamilisha utambuzi wa aina 13 za mbegu za asili za mahindi, mpunga, maharage na papai ambazo zimeingizwa kwenye mfumo rasmi wa mbegu.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Mwamvuli wa kilimo hai(TOAM) Dkt Mwatima Juma amesema kuwa huu ni Mkutano wa wadau kukumbushana, kuwapa nafasi za kuwa na maudhui mbalimbali ya kisayansi,ya kijamii na ya maendeleo ambayo yatazungumzwa na watu kupata nafasi ya kujadiliana.

Na kusema kuwa kilimo hai kinakwenda mbio sana duniani hivyo nao wanatakiwa kukaza kamba kukisukuma kiende mbio zaidi kutokana na mujibu wa masoko.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa  mwamvuli wa Kilimo hai (TOAM) Bwana Bakari Mongo ameeleza kuwa Mkutano huu huwa ni jukwaa muhimu sana kwa wadau mbalimbali wakiwemo wakulima,watafiti,wanazuoni,Wana Habari,Sekta binafsi na pia wabia wa Maendeleo kubadilishana maarifa na uzoefu ambao utasaidia kuendeleza kilimo Ikolojia Hai katila Taifa la Tanzania. 

Kwani katika Mkutano wao huu wa nne wanategemea kuwa na maazimio lakini pia kujipima walipofikia juu ya yale ambayo walikubaliana katika mikutano iliyopita na kuweka maazimio tena yanayolenga zaidi kusukuma gurudumu la kilimo Ikolojia hai katika Taifa.

Awali wakitoa ushuhuda wa mafanikio ya kilimo hai Bwana Manase Noeki kutoka Halmashauri ya Arusha DC amesema kilimo cha Ikolojia hai kimempa manufaa makubwa ikwemo kuendana na mabadiliko ya Tabia nchi na pia namna ya kutunza mazingira kama vile kuweka kingo,kuotesha miti,kuotesha majani na kutumia mbolea za mifugo kwaajili ya kutunza afya ya udongo.

Naye Bi Mercy Meena mkulima kutoka Morogoro amesema kilimo hiki kimemsaidia kulima mazao mbalimbali ambayo yalisemwa hayatostawi katika maeneo yao lakini kwa kufuatilia kilimo Ikolojia hai alikuta yote yakistawi na akitumia mbegu za asili.

Mkutano huu ni wa siku tatu na unaongozwa na kauli mbiu inayosema “Kilimo Ikolojia Hai: Kuimarisha Usalama wa Chakula na Lishe, Uhimilivu na Ustahimilivu wa Kiuchumi”.





 

Mwakilishi wa Jimbo la Kiwani ambae pia ni Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla amewashauri viongozi kujenga utamaduni wa kuwasaidia wananchi hasa katika kipindi cha mwezi mtukufu wa Ramadhani ili kuweka uwiano sawa wa mahitaji.

Ametoa wito huo mara baada ya zoezi la kuwagawa Iftar kwa  wananchi wa jimbo la kiwani shehia ya kendwa yenye nyumba zaidi ya 1156 hafla iliyofanyika kwenye uwanja wa mpira wa Mauuwani Jimbo la Kiwani.

Amesema ataendeleza utamaduni wake wa  kugawa Iftari kwa wananchi wote hasa wenye mahitaji Maalum ili kupunguza ukali wa maisha na kupata chakula katika Mwezi Mtukufu wa Ramadhani.

Amefahamisha kuwa  mwezi Mtukufu wa Ramadhan ni Maalum kwa waumini wa Dini ya kiislamu kufanya matendo mema  yanayompendeza Mwenyezi Mungu,hivyo ni vyema kwa kila mwenye uwezo kutoa na kuwapa wahitaji ili kupata fadhila zilizomo ndani ya mwezi huu.

Aidha, Mhe. Hemed amesema anatarajia kuzifikia shehia zote saba ( 7 )  zilizomo ndani ya Jimbo hilo na kuzipatia Iftari jambo ambalo litaongezea umoja na mshikamano kwa wannachi wa jimbo hilo.

Sambamba na hayo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar amewaomba wafanya biashara kuwasaidia watu wenye mahitaji maalumu wakiweo Masikini, Wajane, Mayatima na watu wasiojiweza hasa katika mwezi mtukufu wa ramadhani ili kuzidi kuzitakada biashara zao na kupata fadhila zilizomo ndani ya mwezi wa ramadhani.

Kwa upande wake mfanya biashara SAID NASSIR NASOR ( BOBAR ) ameishukuru serikali ya mapinduzi ya Zanzibar kwa kuendelea kumpatia ushirikiano ambapo kwa mwezi huu wa ramadhani amepatiwa  usafiri wa kusafirisha bidhaa mbali mbali  ambazo atawakabidhi wananchi wa kisiwani Pemba wakiwemo waannchi wa jimbo la kiwani.

Amesema kuwa lengo lake ni kuwafikia  wananchi mbali mbali wasio na uwezo kwa Unguja na Pemba ili kila mwananchi apate sadaka  itakayowasaidia kwa Iftari lakini pia aweze kupata fadhila hapa duniani na kesho akhera.

Nao wananchi waliopatiwa sadaka hizo wamemshukuru mwakilishi wao kwa kuendelea kuwatumikia kwa  moyo wa upendo,  huruma na usawa kwa wananchi wote jimboni humo jambo ambalo linawapa faraja na imani kubwa juu yake.

Wamesema hawana shaka na utendaji kazi wa Mhe. Hemed na matumaini yao makubwa ni kuzidi kuwaletea maendeleo jimbo humo kama vile alivyoanza kuzitekeleza ahadi mbali mbali alizoziahidi wakati akiomba ridhaa ya kuwa mwakilishi wa Jimbo la Kiwani.













Top News