Na Benny Mwaipaja, Dodoma.

Serikali kupitia Wizara ya Fedha imeliomba Bunge kuidhinisha jumla ya shilingi trilioni 21.3 kwa ajili ya utekelezaji wa majukumu ya Wizara hiyo pamoja na taasisi zake kwa Mwaka wa Fedha 2026/27.

Akiwasilisha Mapendekezo ya Mpango na Bajeti bungeni, Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), alisema fedha hizo zitatumika kugharamia matumizi ya kawaida na maendeleo katika mafungu manane ya Wizara, ambapo kati ya fedha hizo, shilingi trilioni 19.4 zitatumika kwa matumizi ya kawaida huku shilingi trilioni 1.8 zikielekezwa kwenye miradi ya maendeleo.

Alisema kuwa katika Bajeti hiyo, Serikali imepanga kuendelea kusimamia uchumi kwa weledi ili kuhakikisha ukuaji wa uchumi unafikia asilimia 6.3 mwaka 2026 huku mfumuko wa bei ukidhibitiwa kubaki katika katika wigo wa wastani wa asilimia 3 hadi 5.

“Serikali pia inalenga kuimarisha nidhamu ya matumizi ya fedha za umma pamoja na kuongeza ufanisi wa ukusanyaji wa mapato ya ndani” alisema Mhe. Balozi Omar.

Aidha, alibainisha kuwa Wizara imepanga kutenga shilingi bilioni 100 kila mwezi kwa ajili ya kulipa madeni ya watumishi, wakandarasi, wazabuni na watoa huduma ili kupunguza changamoto za malimbikizo ya madeni serikalini.

Kwa upande wa mapato, alisema kuwa Wizara ya Fedha imekadiriwa kukusanya jumla ya shilingi trilioni 55.2, ambapo Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) inatarajiwa kukusanya zaidi ya shilingi trilioni 39.

Katika hatua nyingine, aliliomba Bunge kuiidhinishiwa Ofisi ya Taifa ya Ukaguzi shilingi bilioni 132.2 kwa ajili ya kuimarisha shughuli za ukaguzi wa matumizi ya fedha za umma pamoja na kuendelea na ujenzi wa ofisi zake katika baadhi ya mikoa nchini.

Mhe. Balozi Omar alieleza kuwa bajeti hiyo imeandaliwa kwa kuzingatia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa pamoja na Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025.


TATHMINI YA UTEKELEZAJI WA BAJETI YA 2025/26


Mhe. Balozi Omar alieleza kuwa jumla ya shilingi trilioni 20.18 ziliidhinishwa kwa ajili ya utekelezaji wa matumizi ya kawaida na maendeleo kwa mafungu manane ya wizara hiyo katika mwaka wa fedha 2025/26.

Alisema kati ya fedha hizo, shilingi trilioni 19.43 zilitengwa kwa matumizi ya kawaida ikijumuisha mishahara ya shilingi trilioni 1.10 na matumizi mengineyo ya shilingi trilioni 18.33.

“Bajeti ya maendeleo ilikuwa shilingi bilioni 747.30, ambapo shilingi bilioni 601.70 zilikuwa fedha za ndani na shilingi bilioni 145.60 fedha za nje” Alisema Mhe. Balozi Omar.

Alisema kuwa wakati wa mapitio ya kati ya mwaka, bajeti ya wizara ilihuishwa na kupungua kutoka shilingi trilioni 20.18 hadi shilingi trilioni 19.94, ambapo kati ya kiasi hicho, shilingi trilioni 19.45 zilitengwa kwa ajili ya matumizi ya kawaida na shilingi bilioni 485.99 kwa ajili ya miradi ya maendeleo.

“Hadi kufikia mwisho wa Aprili 2026, wizara ilikuwa imepokea jumla ya shilingi trilioni 14.08 sawa na asilimia 70.63 ya bajeti iliyohuishwa. Matumizi halisi yalifikia shilingi trilioni 14.05, sawa na asilimia 99.76 ya fedha zilizopokelewa” alifafanua Mhe. Balozi Omar.

Wizara pia ilieleza mafanikio yaliyopatikana katika ukusanyaji wa mapato, usimamizi wa deni la Serikali pamoja na ukuaji wa uchumi ambapo katika kipindi cha Julai 2025 hadi Aprili 2026, Serikali ilifanikiwa kukusanya na kutafuta shilingi trilioni 41.37 kutoka vyanzo vya ndani na nje, sawa na ufanisi wa asilimia 82.4 ya lengo la mwaka.

Katika kipindi hicho, Serikali ilitumia shilingi trilioni 9.74 kuhudumia deni la Serikali, ambapo shilingi trilioni 4.45 zilielekezwa kwenye deni la nje na shilingi trilioni 5.29 kwa ajili ya deni la ndani na kwamba ulipaji wa madeni kwa wakati umeendelea kuijengea Tanzania imani katika masoko ya fedha ya kikanda na kimataifa.

“Nina furaha kulijulisha Bunge lako Tukufu kuwa Tanzania imeibuka mshindi wa jumla katika Tuzo ya Usimamizi wa Deni la Umma katika nchi za Jumuiya ya Madola, pamoja na tuzo ya Ofisi Bora ya Usimamizi wa Deni la Serikali katika Kanda ya Afrika” alisisitiza Mhe. Balozi Omar.

Kwa upande wa uchumi, Tanzania ilikua kwa wastani wa asilimia 5.9 mwaka 2025 ikilinganishwa na asilimia 5.5 mwaka 2024. Ukuaji huo umechangiwa na kuongezeka kwa mikopo kwa sekta binafsi, kuimarika kwa miundombinu, shughuli za kilimo, uchimbaji madini, ujenzi pamoja na utekelezaji wa miradi ya kimkakati.

Aidha, alieleza kuwa kiwango cha mfumuko wa bei kiliendelea kubaki katika wastani wa asilimia 3.4 huku akiba ya fedha za kigeni ikifikia dola za Marekani bilioni 5.723, kiasi kinachotosheleza uagizaji wa bidhaa na huduma kutoka nje kwa zaidi ya miezi 4.4

Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akiwasilisha bungeni jijini Dodoma, Mapitio ya Utekelezaji wa Mpango na Bajeti kwa mwaka wa fedha 2025/2026 na Mapendekezo ya Mpango na Bajeti ya Wizara ya Fedha kwa mwaka 2026/2027, ambapo ameliomba Bunge kuidhinisha jumla ya shilingi trilioni 21.3 kwa ajili ya utekelezaji wa majukumu ya Wizara pamoja na taasisi zake kwa Mwaka wa Fedha 2026/27. (Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, WF, Dodoma)
NALA - DODOMA

‎HALMASHAURI ya Jiji la Dodoma imetekeleza ujenzi wa barabara ya lami yenye urefu wa kilomita 1.6 kutoka barabara kuu ya Bahi hadi Hospitali ya Jiji, hatua inayolenga kuboresha huduma za afya na kiuchumi kwa wananchi wa Kata ya Nala.

‎Akizungumza wakati wa uzinduzi wa barabara hiyo, Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa Mwaka 2026, Wazo Mwang’onda alipongeza mradi huo na kusema kuwa ni bora, umekidhi vigezo vyote muhimu kama taratibu za ujenzi wa barabara ya kiwango cha lami zinavyotaka.

‎Alisema kuwa Mwenge wa Uhuru umeridhishwa na ujenzi huo na upo tayari kuizindua. “Mwenge wa Uhuru umeridhishwa na ujenzi huu wa barabara ya Kilomita 1.6 ambayo imekamilika kwa ubora wa hali ya juu na sasa upo kwenye matazamio ya mwisho, umeridhishwa na namna barabara hii imejengwa. Tunaamini wakazi wa eneo hili watanufaika sana na uwepo wa barabara hii" alisema Mwang’onda.

‎Awali akisoma taarifa ya mradi wa ujenzi wa barabara hiyo, Mhandisi wa Miradi katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Mha. Nicodemus Kileo alisema kuwa mradi huo ulitekelezwa na mkandarasi mzawa M/s. Kings Builders Limited kwa gharama ya shilingi bilioni 2.87 zilizotokana na mapato ya ndani ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma, na upo tayari kuzinduliwa.

‎Nae, Mkazi wa Nala, Gervazi Sebastian alipongeza ujenzi wa barabara hiyo akieleza kuwa imeondoa adha ya usafiri kwa wakazi wa Nala. "Tunaishukuru sana serikali kwa kutujengea hii barabara, awali ilikuwa ngumu kupata usafiri wa nafuu kwasababu barabara ilikua mbovu. Kwakweli serikali imetuokoa hata huduma zingine zinapatikana kwa urahisi" alisema Sebastian.

‎Katika hatua nyingine, Mkazi wa Mtaa wa Segu Chini, Asia Omari alipongeza ujenzi wa barabara hiyo akisema kuwa imekuwa mkombozi kwa watumiaji hasa wanawake wajawazito wanaopita kwenda kupata matibabu katika Hospitali ya Jiji la Dodoma.

‎Mradi huo ni miongoni mwa miradi iliyozinduliwa na kuwekewa jiwe la msingi na Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa Mwaka 2026 uliobeba kaulimbiu isemayo “Tanzania ni Yetu Sote, Tushikamane kwa Pamoja Kuleta Maendeleo”.




Na Janeth Raphael MichuziTv - Bungeni Dodoma

Serikali kupitia Wizara ya Fedha imetangaza vipaumbele vinane (8) vya kimkakati kwa mwaka wa fedha 2026/27, vyenye lengo la kukuza uchumi, kuimarisha nidhamu ya matumizi ya rasilimali za umma, na kulipa madeni.

Vipaumbele hivyo vimewasilishwa bungeni na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), wakati akisoma mapendekezo ya mpango na bajeti ya wizara hiyo.Sera na mikakati hiyo mikuu imegawanyika katika maeneo yafuatayo:

1. Ukuaji wa Uchumi na Kudhibiti Mfumuko wa BeiWizara imepanga kusimamia uchumi jumla ili ufikie ukuaji wa asilimia 6.3 ifikapo mwishoni mwa mwaka 2026. Aidha, jitihada zitawekwa ili kudhibiti mfumuko wa bei ubaki kwenye viwango vya tarakimu moja (wastani wa asilimia 3.0 hadi 5.0), huku akiba ya fedha za kigeni ikitunzwa kukidhi uagizaji wa bidhaa na huduma kwa angalau miezi minne (4).

2. Nidhamu ya Matumizi na Ukusanyaji MapatoIli kuhakikisha thamani halisi ya fedha za umma inaonekana, serikali itaimarisha nidhamu ya bajeti (fiscal discipline). Hatua hii itahusisha usimamizi madhubuti wa ununuzi wa umma na kupunguza tabia ya kuhamisha fedha kutoka fungu moja kwenda jingine (reallocation between votes).

3. Kuvunja Rekodi ya Mapato (Tsh Bilioni 55,200.75)Katika bajeti kuu ya serikali ya jumla ya shilingi bilioni 62,334.19, Wizara ya Fedha inalenga kuboresha mifumo ya kodi, misaada, na mikopo ili kuchangia shilingi bilioni 55,200.75 kwenye Mfuko Mkuu wa Hazina. Hii ni sawa na asilimia 88.6 ya bajeti yote.

4. Kulipa Madeni na Kuaminika KimataifaSerikali imetenga shilingi bilioni 15,102.80 kwa ajili ya kulipa kwa wakati riba na mitaji ya madeni yanayotarajiwa kuiva. Hatua hii inalenga kulinda mikataba na kuendelea kujenga imani kwa wawekezaji katika masoko ya fedha ya kikanda na kimataifa.

5. Mabilioni ya Kulipa Watumishi na WakandarasiHabari njema kwa wadau wa ndani ni kwamba serikali itakuwa ikitoa shilingi bilioni 100.00 kila mwezi. Fedha hizi zitasaidia kulipa madeni ya watumishi wa umma, wakandarasi, wazabuni, na watoa huduma mbalimbali ili kuchochea mzunguko wa fedha.

6. Usawa wa Mgawanyo wa Fedha kwa HalmashauriKutakuwa na maboresho makubwa kwenye ugawaji wa rasilimali fedha kati ya Serikali Kuu na Serikali za Mitaa (Halmashauri). Mgawanyo huo utazingatia tafiti za kitaalamu ili kuondoa urudufu wa majukumu na kuleta uwiano wa kimaendeleo nchini.

7. Mageuzi ya Mfumo wa Bajeti (PBB)Serikali itafanya tathmini ya kina ya usimamizi wa bajeti kwa kutumia Mfumo wa Programu (Programme Based Budgeting – PBB). Lengo ni kuwezesha maamuzi sahihi ya kimabadiliko katika upangaji wa bajeti unaoleta matokeo ya moja kwa moja kwa wananchi.

8. Matumizi ya Akili Unde (AI) na Utawala BoraKatika kwenda na wakati, wizara itajenga uwezo wa watumishi wake kuhusu masuala ya Mazingira, Jamii na Utawala Bora (ESG). Kubwa zaidi, serikali itaanza kuingiza matumizi ya Akili Unde (Artificial Intelligence - AI) katika usimamizi wa fedha za umma na uchumi ili kuongeza ufanisi na uwazi.





Na Albano Midelo

Wakati wengi walidhani ajali ilizika ndoto zake milele, Deogratius Chami ameandika historia mpya Tanzania kwa kuwa mtu wa kwanza mwenye ulemavu wa kutumia kiti mwendo kufika kilele cha Mlima Kilimanjaro (Uhuru Peak, mita 5,895).

Chami, mzaliwa wa Moshi ambaye hivi sasa ni Mkurugenzi wa Kilimanjaro Disability Royour Tour and Safaris, alifikia mafanikio ya kupanda mlima Kilimanjaro baada ya safari ya siku saba mwaka 2014, na kurudia tena mwaka 2023 kwa siku sita pekee.

Mrajisi wa Ushirika Mkoa wa Ruvuma Venance Msafiri akizungumza siku ya maadhimisho ya siku ya ushirika Duniani ambayo yalifanyika wilayani Nyasa mkoani Ruvuma,amesema ushirika umechangia mafanikio ya mwenye ulemavu huyo baada ya kumpatia mkopo wa maendeleo wa shilingi milioni nane mwaka 2023, hivyo kufanikiwa kuanzisha kampuni hiyo ya utalii..

Amesema Kupitia kampuni hiyo Chami sio tu anautangaza utalii,bali pia anautangaza ushirika na kwamba wanatarajia kumualika mkoani Ruvuma ili aweze kuja kutembelea vivutio vya Mkoa wa Ruvuma hususani wilaya ya Nyasa ambayo ni kitovu cha utalii katika Mkoa.

Akiwa na miaka 13 darasa la sita shule ya msingi Kilimanjaro,Chami alipata ajali mbaya ilimlaza kwa karibu miaka miwili katika Hospitali ya KCMC Moshi. Ndoto zake za kuwa mwanajeshi na mchezaji wa mpira zilionekana kufutika.

Hata hivyo, ushauri wa mwalimu wake wa shule ya msingi ulimgeuza kutoka nafasi ya 129 darasani hadi kuwa miongoni mwa wanafunzi bora, hatua iliyomfikisha hadi Shahada ya Maendeleo ya Jamii na Uchumi kutoka Chuo Kikuu cha Ushirika Moshi mwaka 2013.

Kwa mujibu wa WHO (2023), watu bilioni 1.3 duniani wanaishi na ulemavu, sawa na asilimia 16 ya idadi ya watu wote. Chami amethibitisha kuwa ulemavu si mwisho wa mafanikio bali mwanzo wa njia mpya ya ushindi.


Picha mbalimbali za Deogratias Chami mtanzania wa kwanza mwenye ulemavu kupanda mlima kilimanjaro hadi kileleni  kwa kutumia kiti mwendo ,Chami amepanda mlima kilimanjaro mara mbili mara ya kwanza ilikuwa mwaka 2014 ambapo alitumia siku saba kufikia kileleni na mara ya pili mwaka 2023  akiwa na kampuni yake ya utalii alifanikiwa kupanda mlima kilimanjaro kwa kutumia siku sita hadi kileleni

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiagana na viongozi mbalimbali kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) Jijini Dar es Salaam kabla ya kuondoka nchini, kuelekea Shirikisho la Urusi kwa ziara ya Kitaifa itakayoanza tarehe 3 hadi 5 Juni, 2026 kwa mualiko wa Rais wa Shirikisho la Urusi, Mheshimiwa Vladimir Putin

 

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Deus Sangu amesema Serikali itaendelea kushirikiana na Taasisi za Dini nchini kuimarisha maadili kwa jamii na kukuza maemdeleo.

Mhe. Sangu amesema hayo alipomwakilisha Waziri Mkuu Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba katika hafla ya kumsimika uaskofu mchungaji Daniely Liyaseke wa Kanisa la The Charismatic Episcopal Church of Tanzania, Dayosisi mpya ya Ukanda wa Tanzanite One, iliyofanyika Mei 31, 2026 Kijiji cha Terat, Wilaya ya Simanjiro mkoani Manyara.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Sangu amesema Serikali inatambua na kuthamini mchango wa makanisa katika kuimarisha maadili, mshikamano wa kijamii na maendeleo ya Taifa na itaendeleza ushirikiano huo. Ameongeza kuwa kauli mbiu ya kanisa hilo “Kwa neema ya Mungu, tunajenga Huduma kwa vizazi vya sasa na vijavyo” inaakisi dhamira ya kuwekeza kwa kizazi cha sasa na kijacho.

Vile vile, Mhe. Sangu alisisitiza mambo matatu muhimu kwa Taasisi za dini ziendelee kuombea amani, mshikamano na afya njema kwa viongozi wakuu wa nchi akiwemo Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Kadhalika, amesema Serikali itaendelea kushirikiana na tasasisi za dini katika malezi ya vijana ili kujenga Taifa lenye maadili, upendo na uwajibikaji, pia kuendeleza ushirikiano katika utoaji wa elimu na huduma za kijamii kwa kizazi chenye uzalendo na uwajibikaji.

Aidha, Mhe. Sangu aliongoza harambee ya kuchangia ujenzi wa Kanisa, Ofisi na ununuzi wa gari, ambapo katika harambee hiyo Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba amechangia Shilingi Milioni 15 na Waziri Sangu amechangia Shilingi Milioni 5.

Naye, Askofu Daniely Liyaseke aliwashukuru viongozi wa Serikali, viongozi wa dini na waumini kwa mshikamano na ushirikiano, akisisitiza kuwa “ukiona kobe yupo juu ya mti, ujue kuna aliyempandisha.”

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. James Millya pamoja na Mkuu wa Wilaya ya Simanjiro Mhe. Fakih Lulandala, walipongeza uongozi wa Askofu Liyaseke na kusisitiza kuwa uwepo wa Dayosisi hiyo ni nguzo ya mshikamano wa kijamii na maendeleo ya kiroho.

ATTRACTING pickleball players from more than seven countries, the Tanzania Pickleball Open 2026 tournament backed by Absa Bank Tanzania, underscoring the growing popularity of the sport and Tanzania’s ambitions to become a regional sports and tourism hub.

The five-day tournament, held at the Gymkhana Club grounds in Dar es Salaam, brought together elite pickleball players from Kenya, Uganda, Rwanda, South Africa, the Democratic Republic of Congo, India, Turkey and Dubai for one of East Africa’s largest pickleball competitions.

Organised through a partnership between the Tanzania Pickleball Association (TPA) and the East Africa Racket Sports Club (EARSC), the event featured a corporate prize pool of US$15,000 and premium playing equipment, attracting both international competitors and local spectators.

As the tournament’s title sponsor, Absa Bank Tanzania said its support reflects a broader commitment to youth development, community engagement and the promotion of emerging sports in the country.

Speaking during the closing ceremony, Absa Bank Tanzania Marketing and Communications Manager, Mr Beda Biswalo, said the tournament had demonstrated the growing potential of pickleball to unite communities and create opportunities for young people.

“We are inspired by the remarkable energy, discipline and international talent displayed throughout the tournament,” said Mr Biswalo. “Our partnership reflects a deeper purpose—championing a sport that unites communities while creating meaningful opportunities for young people.”

He encouraged more Tanzanians, particularly youth, to embrace the sport, noting that pickleball offers opportunities for recreation, fitness and professional development.

Sports stakeholders say the rapid growth of pickleball is creating new opportunities for athletes through international rankings, scholarships and participation in an expanding global professional circuit. The sport’s accessibility and relatively low cost have also contributed to its increasing popularity across different age groups.

The tournament's success aligns with Tanzania’s broader efforts to strengthen sports as a contributor to economic growth and tourism. Through support from government institutions and private-sector partners, the country has increasingly hosted regional and international sporting events aimed at showcasing Tanzania as a destination for sports tourism.

“Absa Bank investment in the tournament supports the Government’s agenda of developing sports infrastructure, nurturing local talent and positioning sports as a driver of economic activity. The initiative is in line with ongoing efforts by the National Sports Council (BMT) to expand opportunities for athletes and sports organisations”, Mr Biswalo added.

The bank also acknowledged the contributions of the Government of Tanzania, co-sponsors Pepsi and CBD Hotel, technology partner Courtly, tournament organisers and fans whose support contributed to the successful staging of the championship.

Following the success of the 2026 edition, Absa Bank remains committed to supporting the growth of pickleball and is optimistic that the Tanzania Pickleball Open will continue to attract increased international participation, help develop the next generation of Tanzanian athletes, and elevate the country's profile on the global sporting stage.

On his part, the President of Tanzania Pickleball Association and the East Africa Rackets Sports Club Director, Kartik Kapor, stated that the Tanzania Pickleball Open 2026 was a resounding success and marked only the beginning of Tanzania’s journey toward becoming a global pickleball powerhouse.

During the finals Women’s Doubles, Rakshika/Agni won 1st place, Sally/Rinaaz won 2nd place and Edna/Ester, WON 3rd place. On men’s Double category, Yuvraj/Purvansh won 1st place, Fifi/Shane won 2nd place and Kartik/Dev won 3rd place.

On the Men’s Singles; Purvansh won 1st place, Fifi 2nd and Dev won 3rd place. International Mixed Doubles; Shaheed/Deandra won 1st place, Ahmad/Zainab 2nd and Lisa/Zuber won 3rd place. Open Women’s Singles; Agni won 1st place, Tamara won 2nd and Sally won 3rd place.

On Mix Doubles winners; Rakshika/Dev won 1st place, 2nd place went to Alikhan/Sally and Yuvraj/Agni won 3rd place.
President of Tanzania Pickleball Association and the East Africa Rackets Sports Club Chairman, Kartik Kapor, shakes hands with Absa Bank Tanzania Head of Large Corporates, Christopher Mgani (right), during the closing ceremony of the Tanzania Pickleball Open 2026, sponsored by the financial institution, at the Dar es Salaam Gymkhana Club.
Absa Bank Tanzania Head of Large Corporates, Christopher Mgani (left), presents awards to winners of the Tanzania Pickleball Open 2026 during the closing ceremony at the Dar es Salaam Gymkhana Club. The tournament was sponsored by Absa Bank.



Absa Bank Tanzania Head of Large Corporates, Christopher Mgani (right), presents trophies to one of the winners of the Tanzania Pickleball Open 2026 during the closing ceremony at the Dar es Salaam Gymkhana Club. The tournament was sponsored by Absa Bank.
Pickleball players in action during the finals of the Tanzania Pickleball Open 2026, sponsored by Absa Bank Tanzania, at the Dar es Salaam Gymkhana grounds.

A pickleball player showcases her skills during the finals of the Tanzania Pickleball Open 2026, sponsored by Absa Bank Tanzania, at the Dar es Salaam Gymkhana grounds.

Cheerful winners of the recently concluded Tanzania Pickleball Open 2026 pose during the closing ceremony at the Dar es Salaam Gymkhana Club. The tournament was sponsored by Absa Bank
Na Janeth Raphael MichuziTv Bungeni - Dodoma

Mbunge wa Viti Maalumu, Khadija Shaban Taya, amesema kuwa anawaheshimu wanaume kwa nafasi yao katika jamii kama baba na kaka, lakini ameeleza kuwa sehemu kubwa ya changamoto za mmomonyoko wa maadili inatokana na baadhi ya wanaume kushindwa kutekeleza ipasavyo majukumu yao ya kifamilia, hali inayosababisha wanawake kubeba mzigo mkubwa wa uangalizi wa familia.

Akichangia hoja hotuba ya makadirio ya mapato na matumizi ya wizara ya Maendeleo ya jamii Jinsia Wanawake na Makundi maalum Kwa mwaka wa fedha 2026/27 amesema kuwa pale wanaume wanaposhindwa kusimama katika majukumu yao ya malezi na uongozi wa familia, wanawake hujikuta wakilazimika kutoka na kujitafutia kipato ili kuhakikisha watoto wanapata mahitaji ya msingi.

Amefafanua kuwa hali hiyo imekuwa na athari za kijamii, ikiwemo kuongezeka kwa changamoto za malezi na kuporomoka kwa misingi ya maadili katika baadhi ya familia.

“Kwa hakika hakuna mwanamke mwenye akili timamu anayependa kumuumiza mwanaume anayempenda na kumheshimu. Wanawake wengi wanajikuta wakibeba majukumu makubwa kwa sababu ya mazingira yaliyopo,” amesema.

Aidha, Mbunge huyo ameeleza kuwa kuna baadhi ya wanaume wanaotelekeza familia zao, ikiwemo watoto wenye ulemavu, hali inayosababisha wanawake kuachwa peke yao katika mzigo wa malezi na matunzo.

Ameongeza kuwa katika baadhi ya familia, watoto wenye ulemavu wamekuwa wakikosa msaada wa baba zao, jambo linalosababisha changamoto kubwa kwa akina mama wanaojitahidi kuwalea na kuwahudumia bila msaada wa karibu wa kifamilia, wakati mwingine hata kukumbana na kutengwa na baadhi ya ndugu na jamii.

Katika wito wake kwa Serikali, Khadija Shaban Taya ameiomba kuangalia kwa karibu kundi la watoto wenye ulemavu na wazazi wao, ili kuhakikisha wanajumuishwa kikamilifu katika sera na mipango ya Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, ili kurahisisha upatikanaji wa huduma na utekelezaji wa haki zao.


Na Said Mwishehe,Michuzi TV


KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi(CCM) Dk.Asha-Rose Migiro amejibu maswali mbalimbali aliyoulizwa na Mtangazaji Salim Kikeke kutoka Crown Media.

Kikeke amemuuliza maswali mbalimbali Dk.Migiro ambayo kwa sehemu kubwa yalijikita katika ripoti ya Tume ya kuchunguza vuruga kabla na baada ya Oktoba 29 ambayo iliongozwa na Mwenyekiti wake Jaji Mkuu mstaafu Othman Chande.

Nakuletea maswali matano kati ya maswali mengi aliyoulizwa

Dk.Migiro na kuyajibu kwa ufasaha na weledi mkubwa.Majibu ambayo yanathibitisha uwezo na umahiri wake katika uongozi hasa kwa kutambua historia yake ya uongozi kitaifa na kimataifa.Maswali hayo yalikuwa hivi;


Kikeke:Chama Cha Mapinduzi kimekuwa kimya kwa muda mrefu tangu ripoti ya Jaji chande kutoka, kwanini imekuwa kimya na kwanini sasa mmekubali kuzungumza na sisi?

Dk.Migiro: Ningependa kuliweka jambo hili katika muktadha sahihi , mtambuka vurugu za Oktoba 29 ni tukio ambalo lilitusitua wengi na sisi wana CCM tulishutuka zaidi kwani haijawahi kutokea katika taifa letu.

Tulipata mshangao, kulikuwa na kuduwaa na kulikuwa na kutafuta muda wa kulitafakari kwa kina nini kimetupata sisi Tanzania baada ya miaka mingi ya kuwa nchi yenye utulivu, amani na mshikamano

Kwahiyo ilichukua muda, na ilituhitaji kuitafakari hotuba ile ya Jaji Chande ambayo ilitokana na kazi waliyoifanya yeye na wana Tume wenzake.Kwahiyo ilichukua muda lakini baadae Chama kilizungumza kidogo kupitia Katibu wa Itikadi na Uenezi Kenani Kihongosi

Naye alisema wazi kwanza tunapongeza kuanzishwa kwa tume ile ilikuwa hatua muhimu katika kurejesha nchi yetu kwenye mstari.Pili alishukuru tume kwa kazi waliyofanya , kazi ambayo wameifanya kwa weledi mkubwa na mpaka sasa inaendelea kuwa sehemu ya namna ya sisi kubaini nini kilitokea na twendeje

Vilevile aliwashukuru wananchi , kwasababu kazi ya tume isingekamilika kama wananchi wasingejitokeza wakaunga mkono, wakatoa maoni yao.Kwahiyo ilikuwa hatua muhimu.

Lakini leo hii umetaka kuongea na sisi ni fursa nzuri na wakati muafaka na mimi Katibu Mkuu kueleza zaidi kuhusu muelekeo wetu kama Chama Cha Mapinduzi kuhusu taarifa ile twendeje kama Taifa na mengineyo ambayo utaona yanafaa

Kikeke:Umezungumza aliyosema Katibu Mwenezi,mnaunga mkono taarifa iliyotolewa na Tume ya Jaji Chande?


Dk.Migiro: Kwanza CCM tumepokea taarifa hii kwa umakini mkubwa na kwa kujua kwamba ni hatua muhimu sana tunataka kujua nini kilitokea kwasababu tunataka suala hili lisijirudie na Chama Cha Mapinduzi kingependa kufuatilia kwa karibu sana hatua gani zitafuata baada ya tume kutoa taarifa yake.Ni wakati muafaka kabisa kwa sisi CCM kuzungumza kupitia sauti ya Katibu Mkuu

Kikeke: Chama Cha Mapinduzi katika mkutano wake wa Halmashauri Kuu Taifa walionekana kuvipongeza vyombo vya ulinzi na usalama katika matukio ya Oktoba 29 , watu waliuawa katika siku ile ,kwanini mlifanya vile?


Dk.Migiro:Kwanza kabisa niseme tunaendelea kuonesha masikitiko yetu makubwa sana kwa vifo vilivyotokea .Vinapotokea vifo au hata kifo kimoja ni suala zito .Katika taarifa yake Mheshimiwa Jaji Chande alieleza kwamba tume ilibaini kuna watu takribani 518 waliopoteza maisha pamoja na madhara mengine yamejitokeza.

Kwahiyo Chama Cha Mapinduzi tunachukua hili suala kwa masikitiko makubwa sana na wako wengine wanaosema idadi hiyo ni ndogo labda ingekuwa kubwa lakini tutakumbuka tume ilitueleza na sisi Chama Cha Mapinduzi hatuna sababu ya kutia shaka vyanzo vyao ndio viliwapa taarifa ile.

Walisema walipata taarifa kupitia hospitali binafsi ,hospitali za serikali, Msajili wa Vizazi na vifo.Zote hizi zimeonesha watu 518 ndio waliopoteza maisha lakini walitutahadharisha inawezekana idadi ile ikabadilika kwasababu wako ambao hawakwenda hospitali wala hawakuandikisha.Sasa kwa Chama Cha Mapinduzi uhai wa mtu mmoja ni uhai mkubwa ambao hatuwezi kupima kwa namba

Kwa maana hiyo tumesikitika sana. Sasa kuhusu vyombo vya ulinzi na usalama ndugu Kikeke unafahamu katika nchi yeyote na Tanzania haina tofauti ,vyombo vya ulinzi na usalama vina kazi zake, vina jukumu ,tukizungumzia Polisi mojawapo ya majukumu yake makubwa ni kulinda usalama wa raia na mali zao.

Jeshi la Wananchi wa Tanzania linakazi kubwa ya kulinda mipaka ya nchi yetu,majukumu yake ya msingi ndio hayo sio kuua wananchi na tunafahamu tarehe 29 Oktoba nchi nzima tulikuwa na vituo vya kupigia kura takribani 99,000.

Na kwakuwa tuliamka katika hali ya kawaida wenzetu wanaolinda usalama wa raia walikuwa tayari wamekaa kwenye maeneo ya kupiga kura kwasababu wananchi waliowengi walikuwa wamejitayarisha kutoka kwenda kupiga kura na kurejea nyumbani.

Sasa ilipotokea kadhia ile vyombo hivi na hasa polisi walilazimika kujigawa huku usalama uendelee kuwepo kwenye maeneo ya kupiga kura na huku waje katika yale maeneo yaliyokuwa na fujo na pia itakumbukwa fujo hii ilikuwa kama moto wa nyikani , pale fujo huku fujo,sio Dar es Salaam peke yake ni katika nchi nzima kwa ujumla.

Kwahiyo hawa walikuwa kama wana jambo kubwa la kufanya kuhakikisha kura zinaendelea kupigwa na vile vile usalama katika maeneo mengine.Hilo lilikuwa jukumu lao kubwa na walilifanya na tunaamini kama wasingefanya vile labda madhara yangekuwa makubwa zaidi katika taifa letu.

Na pili ambalo naweza kuliunganisha hapo kwanini pia Chama Cha Mapinduzi kupitia halmashauri kuu tuliwapongeza. Kwasababu kazi waliyoifanya ndio imefanya taifa letu liwe imara mpaka leo pamoja na ile fujo ambayo kwanza hatukuitegemea lakini pia haijwahi kutokea.

Kwahiyo ilitushangaza wote tukapigwa na butwaa na kitu ambacho ningependa tutenganishe hapa inawezekana katika utendaji wa kazi zao kukawa na dosari hiyo inatokea, sasa tusichanganye majukumu yao ya msingi.Kazi nzuri waliyoifanya ya kutunza amani kwa kiwango kile ambacho kilihitajika kwa wakati ule na dosari moja moja zinazojitokeza…

Na hapa sisemi vifo ni dosari ndogo, sio dosari ndogo ni kubwa lakini ndio sababu kuna haja sasa ya kuangalia mazingira ya vifo vile lakini haindoi ukweli kazi waliyofanya ni ya kutukuka katika Taifa letu.


Kikeke:Mheshimiwa Katibu Mkuu inaonekana kama vile vyombo vya dola na hasa polisi vinaingia kwenye siasa kama kukilinda Chama Cha Mapinduzi ,kwanini?


Dk.Migiro:Hebu niambie siasa gani Jeshi la Polisi inafanya ikiashiria wanakilinda Chama Cha Mapinduzi?


Kikeke :Inaonekana kama inazuia wananchi wasitekeleze haki zao kwa kukitetea Chama.

Dk.Migiro:Si kweli ,kwanza kwa kuwa tunazungumzia masuala ya chaguzi ningependa kukumbusha katika mchakato wote wa uchaguzi katika Jamhuri ya Muungano, iwe Bara au Zanzibar hakukua na hali ambayo Jeshi la Polisi ililazimika kuingia kutuliza fujo au kudhibiti waliokuwepo.

Hii inaonesha vyama vyote vilifanya shughuli zao kwa utulivu kabisa na utakumbuka Mwenyekiti wetu wa Chama Cha Mapinduzi Dk.Samia Suluhu Hassan ambaye pia ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania siku ya uzinduzi wa kampeni alisema tunataka tufanye kampeni za kistaarabu,za tulivu ili kuwapa wananchi fursa ya kusikiliza Ilani ya vyama vyetu kusikiliza jinsi tunavyonadi sera zetu, na ahadi zetu na hatimaye siku ikifika wapige kura.

Kwa maana hiyo kulikuwa na utulivu nchi nzima, kwahiyo hapo sioni Chama Cha Mapinduzi kimelindwa vipi lakini kama nilivyosema mwanzo vyombo hivi ni vya taifa na vinawajibu kwa wananchi wake wote wakiwemo wanachama wa Chama Cha Mapinduzi na vyama vingine.


Kikeke:Taarifa ya Tume imesema watu waliuawa kwa kupigwa risasi Oktoba 29 , kwanini mpaka sasa hakuna viongozi wa Serikali ya CCM ambao wamewajibika?

Dk.Migiro:Awali ya yote ninawajibu wa kusema Chama Cha Mapinduzi na Watanzania walio wengi taarifa za kifo zimetusikitisha sana , Jaji Chande alipokuwa anazungumza ametoa takwimu kuna watu takribani 518 ambao waliuawa.

Namba ambayo inatusononesha na alisema inaweza kuongezeka na walitupa vyanzo vyao kwamba kulikuwa na taarifa za hospitali binafsi ,hospitali za Serikali , Msajili wa Vizazi na Vifo ndio zilitoa namba hizi na wamesema inawezekana namba hii ikabadilika kwasababu wako ambao hawakwenda hospitali wala hawakwenda kusajili vifo.

Kikeke: Lakini Mheshimiwa Balozi swali langu lilikuwa kwanini hakuna mtu ndani ya Serikali ya Chama Cha Mapinduzi ambaye amewajibika mpaka hivi sasa kwa yaliyotokea?

Dk.Migiro:Uwajibikaji ni suala muhimu sana na sisi Chama Cha Mapinduzi matumaini yetu yako kwenye tume ya uchunguzi wa jinai ambayo kazi yake itatoa mwanga zaidi katika suala la uwajibikaji ni muhimu .Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi Dk.Samia Suluhu Hassan ambaye pia ni Rais wa Jamhuri ya Muungano alieleza wazi hakuna mtu aliyejuu ya sheria.

Kwa maana hiyo suala la uwajibikaji linanafasi kubwa sana ndani ya Chama Cha Mapinduzi na msisitizo huo tumeupata sio tu kwenye taarifa ya Tume na hata kwa kiongozi mkuu wa taifa letu .



Kama vipi tuwasiliane tupige stori
kuhusu majibu ya Dk.Migiro
0713833822





Mkurugenzi wa Huduma za Mifugo wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Dkt. Benezeth Lutege, akizungumza wakati wa ufunguzi wa Warsha ya Uandaaji wa Rasimu ya Mkakati wa Kitaifa wa Mawasiliano Wakati wa Dharura kwa Huduma za Mifugo Tanzania, kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bi. Agness K. Meena. Warsha hiyo imefanyika leo Juni 1, 2026, katika Ukumbi wa Masailand Hall jijini Arusha.



Mkurugenzi Msaidizi wa Epidemiolojia na Magonjwa ya Mifugo Yanayovuka Mipaka (TADs) akitoa mchango wake katika majadiliano ya Warsha ya Uandaaji wa Rasimu ya Mkakati wa Kitaifa wa Mawasiliano Wakati wa Dharura kwa Huduma za Mifugo Tanzania, iliyofanyika leo Juni 1, 2026, jijini Arusha.



Afisa Habari II wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bi. Chiku Makwai, akitoa mchango wake katika majadiliano ya Warsha ya Uandaaji wa Rasimu ya Mkakati wa Kitaifa wa Mawasiliano Wakati wa Dharura kwa Huduma za Mifugo Tanzania, iliyofanyika leo Juni 1, 2026, jijini Arusha.



Afisa Sheria I wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bw. Denis Ukaka, akitoa mchango wake katika majadiliano ya Warsha ya Uandaaji wa Rasimu ya Mkakati wa Kitaifa wa Mawasiliano Wakati wa Dharura kwa Huduma za Mifugo Tanzania, iliyofanyika leo Juni 1, 2026, jijini Arusha.



Na Chiku Makwai – ARUSHA

Shirika la Afya ya Wanyama Duniani (WOAH), kwa kushirikiana na Wizara ya Mifugo na Uvuvi, limeanza mchakato wa kuandaa Rasimu ya Mkakati wa Kitaifa wa Mawasiliano Wakati wa Dharura kwa Huduma za Mifugo Tanzania, hatua inayolenga kuimarisha uwezo wa nchi katika kuzuia, kudhibiti na kukabiliana na milipuko ya magonjwa ya mifugo.

Warsha ya kuandaa rasimu hiyo imefunguliwa leo, Juni 1, 2026, katika Ukumbi wa Masailand Hall jijini Arusha na Mkurugenzi wa Huduma za Mifugo, Dkt. Benezeth Lutege, kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Mhe. Agness K. Meena.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa warsha hiyo, Dkt. Lutege amesema mawasiliano yenye ufanisi ni nyenzo muhimu katika kudhibiti na kukabili milipuko ya magonjwa ya mifugo kwa kuwa huwezesha utoaji wa taarifa sahihi kwa wakati kwa wadau wote wanaohusika.

Amesema Serikali inaendelea kuimarisha mifumo ya tahadhari na mwitikio wa haraka ili kuhakikisha magonjwa ya mifugo yanagunduliwa na kudhibitiwa mapema kabla hayajasababisha athari kubwa kwa uzalishaji, biashara ya mifugo na afya ya jamii.

“Mkakati huu utaweka msingi wa kuwa na mfumo mmoja wa kitaifa wa mawasiliano ya dharura utakaoongoza utoaji wa taarifa, ushirikishwaji wa wadau na usimamizi wa mawasiliano wakati wa matukio ya milipuko ya magonjwa ya mifugo,” amesema Dkt. Lutege.

Aidha, amebainisha kuwa magonjwa mbalimbali ya mifugo, ikiwemo Homa ya Bonde la Ufa (Rift Valley Fever), yanahitaji uratibu madhubuti wa mawasiliano ili kuhakikisha wananchi na wadau wanapata taarifa sahihi zitakazowawezesha kuchukua hatua stahiki kwa wakati.

Warsha hiyo imewakutanisha wataalamu wa mifugo, afya ya wanyama, mawasiliano na wadau wengine kutoka taasisi za Serikali pamoja na mashirika ya kimataifa kwa lengo la kujadili mbinu bora za mawasiliano ya hatari, usimamizi wa taarifa za dharura na mikakati ya kuimarisha mwitikio wakati wa milipuko ya magonjwa.

Washiriki pia wanatarajiwa kujadili matumizi ya teknolojia za kisasa katika utoaji wa taarifa pamoja na namna ya kuimarisha ushirikiano kati ya sekta ya afya ya wanyama na afya ya binadamu kwa kuzingatia dhana ya Afya Moja (One Health).

Kupitia warsha hiyo, Tanzania inatarajia kuwa na mkakati madhubuti wa mawasiliano ya dharura utakaosaidia kuimarisha mifumo ya tahadhari ya mapema, kuongeza mwitikio wa haraka wakati wa matukio ya dharura na kulinda ustawi wa mifugo sambamba na kuchangia maendeleo ya uchumi wa taifa.



MBUNGE wa Kisarawe, Dkt. Selemani Jafo,akichangia hotuba ya Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum leo Juni 1,2026 bungeni jijini Dodoma.



MBUNGE wa Kisarawe, Dkt. Selemani Jafo,akichangia hotuba ya Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum leo Juni 1,2026 bungeni jijini Dodoma.

......

MBUNGE wa Kisarawe, Dkt. Selemani Jafo, ameitaka Serikali kuboresha mazingira ya kazi kwa Maafisa Maendeleo ya Jamii nchini ikiwemo kuwapatia magari ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi.

Akichangia hotuba ya Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum bungeni, Dkt. Jafo amesema maafisa hao ni nguzo muhimu katika kusukuma maendeleo ya jamii na wanastahili kuwezeshwa kwa vitendea kazi vinavyokidhi mahitaji ya kazi zao.

Amesema Maafisa Maendeleo ya Jamii ni mawakala wa mabadiliko katika jamii kwa kuwa karibu kila programu ya maendeleo inayotekelezwa nchini inahitaji ushiriki wao wa moja kwa moja, hivyo ni muhimu kupewa heshima na mazingira bora ya kufanyia kazi.

Dkt. Jafo ameeleza kuwa pamoja na magari, maafisa hao wanapaswa kuwa na ofisi zenye hadhi na rasilimali za kutosha zitakazowawezesha kuwafikia wananchi kwa urahisi na kutoa huduma stahiki.

Aidha, ameishauri Serikali kuanzisha vitengo vya Maendeleo ya Jamii katika wizara zote na taasisi za umma zaidi ya 325 ili kuhakikisha masuala ya maendeleo ya jamii yanapewa kipaumbele na kuratibiwa kwa ufanisi katika sekta mbalimbali.

Pia amependekeza kuanzishwa kwa Kitengo cha Uratibu wa Sekta ndani ya Wizara ya Maendeleo ya Jamii kitakachosaidia kuunganisha taarifa za maendeleo kutoka wizara na taasisi mbalimbali, hatua ambayo alisema itaiwezesha nchi kuwa na mfumo imara wa kufuatilia maendeleo ya wananchi na taifa kwa ujumla.

Na Janeth Raphael MichuziTv - Bungeni Dodoma 

Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dkt. Dorothy Gwajima, amesema Serikali imeweka mkazo mkubwa katika malezi, makuzi na ustawi wa watoto kama msingi wa kujenga Taifa lenye maadili, mshikamano na maendeleo endelevu kuelekea utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Akiwasilisha bungeni hotuba ya mapitio ya utekelezaji wa Mpango na Bajeti ya mwaka 2025/26 pamoja na makadirio ya mapato na matumizi kwa mwaka 2026/27, Dkt. Gwajima alisema Wizara yake imejipanga kutekeleza vipaumbele saba vya kimkakati vitakavyochochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi kwa manufaa ya Watanzania wote.

Ameeleza kuwa katika mwaka wa fedha 2026/27, Wizara itajikita katika maeneo yenye uwezo mkubwa wa kuleta mageuzi ya kijamii na kiuchumi, huku ikilenga kujenga Tanzania yenye jamii imara, jumuishi na inayozingatia maendeleo endelevu.

Kwa mujibu wa Waziri huyo, kipaumbele cha kwanza kitakuwa ni kujenga mtaji watu wa Taifa na kuandaa kizazi cha Tanzania ya mwaka 2050 kitakachozingatia maadili, uzalendo, haki, usawa, ustawi na maendeleo jumuishi. Alisema Serikali inaamini kuwa watu ndiyo rasilimali muhimu zaidi katika safari ya maendeleo ya Taifa.

Aidha, amebainisha kuwa Serikali itaendelea kuimarisha huduma za ustawi, malezi na makuzi ya watoto pamoja na mifumo ya ulinzi wa kijamii ili kuhakikisha kunakuwa na Taifa lenye mshikamano, uthabiti na utu wa kibinadamu.

Katika eneo la usawa wa kijinsia, Dkt. Gwajima amesema Serikali itaendelea kuimarisha mifumo ya uwezeshaji wa wanawake na kupambana na vitendo vya ukatili wa kijinsia ili kuhakikisha wanawake wanashiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo na uchumi wa Taifa.

Pia ameeleza kuwa Wizara inalenga kufanya mageuzi ya kiuchumi kwa makundi maalum na sekta isiyo rasmi kwa kuwasaidia wananchi kutoka katika uchumi wa kujikimu na kuingia katika uchumi rasmi wa kibiashara wenye tija, ushindani na mchango mkubwa katika pato la Taifa.

Kwa upande wa matumizi ya teknolojia, Waziri huyo alisema Serikali itaongeza matumizi ya mifumo ya kidijitali na takwimu katika utoaji wa huduma za kijamii ili kurahisisha utendaji kazi na kuhakikisha maamuzi yanafanyika kwa kuzingatia ushahidi wa kitakwimu.

Ameongeza kuwa juhudi pia zitaelekezwa katika kujenga jamii yenye amani, uwajibikaji na mshikamano pamoja na kuimarisha ushirikiano wa kimkakati kati ya Serikali, Asasi za Kiraia, sekta binafsi, taasisi za dini na wadau wa maendeleo.

Dkt. Gwajima amesema kupitia vipaumbele hivyo, Serikali inalenga kujenga jamii salama na yenye ustawi, wanawake wenye nguvu kiuchumi, watoto waliopata malezi bora, pamoja na uchumi jumuishi unaochochewa na maarifa, teknolojia na ubunifu.

Amesisitiza kuwa bajeti ya Wizara hiyo imeweka kipaumbele katika huduma za ustawi wa jamii, uratibu wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali, huduma kwa watoto, wazee, wanawake, wanaume na makundi mengine maalum, akibainisha kuwa huduma hizo ni sehemu muhimu ya kulinda amani, usalama na uthabiti wa Taifa.

“Hatutapima mafanikio ya bajeti hii kwa kiasi cha fedha kilichotumika pekee, bali kwa matokeo yatakayopatikana kwa familia, wananchi na Taifa kwa ujumla,” alisema.

Katika sehemu ya hotuba yake iliyovuta hisia za wabunge, Waziri huyo aliweka msisitizo mkubwa kwenye suala la malezi ya watoto, akisema ndilo jambo linalobeba mustakabali wa Tanzania kuliko jambo jingine lolote.

Ameeleza kuwa pamoja na uwekezaji mkubwa unaofanywa na Serikali katika miundombinu mbalimbali ikiwemo reli za kisasa, bandari, viwanja vya ndege na miji ya kisasa, mafanikio hayo hayatakuwa na maana ikiwa Taifa litashindwa kujenga watoto wenye maadili, nidhamu, uzalendo, utu na uwezo wa kushindana katika dunia ya mwaka 2050.

“Taifa lolote hujengwa kwanza kwenye malezi kabla halijajengwa kwenye uchumi. Mtoto wa leo ndiye mtendaji wa Serikali wa kesho, daktari wa kesho, mwalimu wa kesho, jaji wa kesho, askari wa kesho, mwekezaji wa kesho na kiongozi wa Taifa wa kesho,” alisema.

Ameonya kuwa kuharibu malezi ya watoto wa leo ni sawa na kuharibu Tanzania ya kesho, akisisitiza umuhimu wa familia, jamii na taasisi mbalimbali kushiriki kikamilifu katika kuhakikisha watoto wanalelewa katika misingi ya maadili mema, uzalendo na uwajibikaji.

Dkt. Gwajima alihitimisha kwa kueleza kuwa utekelezaji wa mpango na bajeti ya mwaka 2026/27 umeandaliwa mahsusi kuleta matokeo yanayopimika, kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma, kupunguza umaskini, kulinda makundi yaliyo hatarini na kuimarisha mshikamano wa Kitaifa kuelekea kufanikisha Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.






-Yalenga Kuimarisha Ufanisi wa Chama

Na Oscar Assenga,TANGA

Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Tanga kimeongeza kasi ya utekelezaji wa mradi wake wa ujenzi wa nyumba 36 za watumishi baada ya Mwenyekiti wa chama hicho mkoani humo, Rajab Abdulrahman, kukabidhi shilingi milioni 500 kwa ajili ya kukamilisha mradi huo unaotekelezwa katika wilaya tisa za mkoa huo.

Fedha hizo zilikabidhiwa kwa Katibu wa CCM Mkoa wa Tanga, Mfaume Kizigo, katika hatua inayodhihirisha dhamira ya chama ya kuboresha mazingira ya kazi na makazi kwa viongozi wake wa ngazi za wilaya.

Akizungumza wakati wa makabidhiano hayo, Rajab alisema mradi huo unatarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Desemba mwaka huu na kwamba utakuwa na mchango mkubwa katika kuimarisha utendaji wa watumishi pamoja na shughuli za chama katika maeneo mbalimbali ya mkoa.

Alieleza kuwa mradi huo una thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 2.5, huku fedha zote zinazohitajika kwa ajili ya utekelezaji wake zikiwa tayari zimepatikana kupitia michango ya wanachama, viongozi na wadau mbalimbali wa chama.

"Mradi huu unagharimu jumla ya shilingi bilioni 2, milioni 500 na laki 250. Fedha hizi zimepatikana kupitia michango mbalimbali ikiwemo milioni 56 zilizotolewa awali, milioni 10 kutoka kwa MNEC pamoja na michango iliyokusanywa kutoka wilaya zote za mkoa," alisema Rajab.

Mwenyekiti huyo alibainisha kuwa kukamilika kwa nyumba hizo kutasaidia kutatua changamoto za makazi kwa baadhi ya viongozi wa chama katika ngazi ya wilaya, jambo litakaloongeza utulivu wa kazi, uwajibikaji na ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.

Alisema nyumba hizo si tu kwamba zitakuwa makazi ya viongozi, bali pia ni uwekezaji wa muda mrefu wa chama katika kujenga taasisi imara yenye uwezo wa kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi na kuendelea kuwahudumia wanachama wake.

"Tunajenga misingi ya chama kwa vizazi vya sasa na vijavyo. Viongozi wanaweza kubadilika, lakini miundombinu tunayojenga leo itaendelea kulitumikia chama kwa miaka mingi ijayo," alisisitiza.

Rajab aliongeza kuwa ujenzi wa chama ni jukumu endelevu linalohitaji mshikamano wa wanachama wote, akisisitiza kuwa maendeleo ya chama hayawezi kupatikana bila ushiriki wa pamoja wa wanachama wake.

Kutokana na hilo, aliwataka wana-CCM wa Mkoa wa Tanga kuendelea kuchangia kwa hali na mali, kutumia elimu na uzoefu wao pamoja na nguvu kazi katika kukiimarisha chama.

Kwa upande wake, Katibu wa CCM Mkoa wa Tanga, Mfaume Kizigo, alisema mradi huo ni sehemu ya mkakati wa muda mrefu wa chama wa kuimarisha utendaji wake katika ngazi za wilaya kwa kuhakikisha viongozi wanapata mazingira bora ya kazi na makazi.

Alifafanua kuwa kila wilaya imepangiwa kujenga nyumba nne ambazo zitatumika na viongozi muhimu wa chama na jumuiya zake.

"Kila wilaya imepangiwa kujenga nyumba nne ambazo ni nyumba ya Katibu wa CCM wa Wilaya, nyumba ya Katibu wa Jumuiya ya Vijana, nyumba ya Katibu wa Jumuiya ya Wazazi pamoja na nyumba ya Katibu wa UWT," alisema Kizigo.

Alieleza kuwa uwepo wa nyumba hizo utasaidia kupunguza gharama za upangaji wa makazi, kuimarisha upatikanaji wa viongozi katika maeneo yao ya kazi na kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa shughuli za chama na jumuiya zake.

Kwa mujibu wa Kizigo, kukamilika kwa mradi huo kutakuwa hatua muhimu katika kuijengea CCM Mkoa wa Tanga miundombinu imara itakayosaidia kuendeleza shughuli zake za kisiasa, kiutawala na kijamii kwa ufanisi zaidi katika miaka ijayo.

Mradi wa Jenga Kesho Iliyo Bora (BBT) ya Unenepeshaji wa Mbuzi na Kilimo cha Malisho, ambao unatekelezwa na Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kushirikiana na Wizara ya Kilimo, umepanga kuwawezesha wanawake na vijana 6000 ndani ya muda wake wa utekelezaji wa Miaka Mitano wa Mradi huo, ambao ukiwa na lengo la kuongeza ushiriki wa wanawake na vijana katika ujasiliamali wa Biashara ya Mifugo.

Akizungumza leo Juni 1, 2026 Mkoani Morogoro, katika Warsha ya Upitiaji, Uhakiki wa Uwasilishaji wa Ripoti ya awali ya Jinsia na Ujumuishaji wa Kijamii katika Programu hiyo ya BBT, Meneja Mradi wa BBT Upande wa Jinsia na Ujumuishaji wa Kijamii, Bi. Neema Urassa amesema Mradi huo una lengo la kuwawezesha Wanawake na Vijana kupitia shughuli za unenepeshaji wa Mbuzi na Kondoo kibiashara pamoja na Kilimo cha Malisho ya Mifugo.

"Mradi huu unawalenga zaidi Wanawake na vijana, ambao kupitia Mradi huu watapata kujifunza vitu mbalimbali kwa vitendo katika mnyororo mzima wa thamani wa mazao ya mifugo, hususan mbuzi na Kondoo na Kilimo cha Malisho ya Mifugo, ili baadae wawe na uwezo wa kuingia kwenye biashara za unenepeshaji wa mifugo kwa lengo la kujiongezea kipato pamoja na kuchangia ukuaji wa uchumi wa taifa." Amesema Bi. Urassa

Aidha, Bi. Urassa amesema baada ya vijana kupata ujuzi huo, matarajio ya Serikali ni kuwa vijana wataweza kujiajiri wenyewe, kuanzisha biashara zao, na kuwa sehemu ya suluhisho la changamoto ya ajira nchini, ambapo vijana watakaonufaika watakuwa na fursa ya kupatiwa mikopo isiyo na dhamana kwa ajili ya kuendeleza biashara zao baada ya mafunzo.

Vilevile, Bi. Urassa,  ameweka wazi kuwa Mradi huo unatokana na Uongozi madhubuti wa Serikali ya Awamu ya Sita wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kutambua kwa kina changamoto ya ukosefu wa ajira miongoni mwa vijana, ndiyo maana Mheshimiwa Rais amechukua juhudi za makusudi kuhakikisha fedha hizo zinapatikana kwa ajili ya kuboresha maisha ya vijana kupitia miradi yenye tija kama huo wa BBT ambao unaendana na Dira ya Taifa ya Mwaka 2050.








Top News