KATIKA maadhimisho ya Siku ya Familia Duniani, wito umetolewa kwa familia za Tanzania kuzingatia uzazi wa mpango kama njia muhimu ya kujenga familia imara, kukuza uchumi na kuhakikisha watoto wanapata malezi bora yatakayowawezesha kufikia ndoto zao.

Imeelezwa kuwa familia ndiyo taasisi ya msingi katika ujenzi wa taifa, uchumi na maendeleo ya nchi yoyote duniani, lakini changamoto ya ongezeko kubwa la watu imeendelea kuwa kikwazo kwa familia nyingi kumudu gharama za malezi, elimu na afya kwa watoto.

Takwimu zinaonesha kuwa Tanzania ina ongezeko la watu linalozidi asilimia tatu kwa mwaka, kiwango ambacho ni kikubwa kuliko wastani wa Bara la Afrika wa asilimia mbili na wastani wa dunia wa asilimia moja. Hali hiyo imeelezwa kuongeza mzigo wa utoaji wa huduma za kijamii huku taifa likikabiliwa na changamoto ya kujenga rasilimali watu yenye ubora.

Kwa mujibu wa tathmini ya maendeleo ya uchumi, Tanzania kwa sasa ipo nafasi ya 81 kwa ukubwa wa uchumi duniani na ya 165 kwa pato la mtu mmoja, huku ikiwa nafasi ya 20 kwa idadi ya watu duniani. Makadirio yanaonesha kuwa ifikapo mwaka 2050, idadi ya watu inaweza kufikia takribani milioni 137, jambo litakalohitaji uwekezaji mkubwa katika elimu, afya na ajira ili kuhakikisha wananchi wanapata maisha bora.

Aidha, imeelezwa kuwa nchi kama China zilipata mafanikio ya haraka ya kiuchumi kutokana na sera za kudhibiti ongezeko la watu, huku India ikiwa na changamoto ya pato la mtu mmoja licha ya kuwa miongoni mwa mataifa yenye uchumi mkubwa duniani. Hali hiyo imeelezwa kuwa somo kwa Tanzania katika kupanga ukuaji wa uchumi unaokwenda sambamba na ukuaji wa watu.

Wadau wa maendeleo wameeleza kuwa ili Tanzania ifikie malengo ya maendeleo ya muda mrefu, kuna haja ya kujenga familia zenye watoto wachache lakini wenye afya, maadili, elimu na maarifa yatakayowawezesha kushindana katika soko la dunia. Pia imesisitizwa kuwa uwekezaji katika sekta za elimu na afya hauwezi kutegemea kodi na mikopo pekee, bali unahitaji ushirikiano wa sekta ya umma na binafsi (PPP) ili kuhakikisha kizazi kijacho kinakuwa nguvu kazi yenye tija kwa taifa.

 


Na Mwandishi wetu- MBEYA

Mkurugenzi msaidizi wa Kituo cha Taifa cha Operesheni na Mawasiliano  ya Dharura kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Bi. Jane Kikunya amewataka Wajumbe wa Timu  ya kukabiliana na Dharura na Uendeshaji  wa Kitio  cha Operesheni  na Mawasiliano  ya Dharura ya  Mkoa wa  Mbeya kufanya kazi kwa ushirikiano, mshikamano na mawasiliano ya karibu ili kutekeleza wajibu wao kwa weledi na ufanisi unaotakiwa.

Mkurugenzi huyo, ameyasema hayo wakati akifungua mafunzo ya siku tano yanayolenga kuziandaa timu za kukabiliana na Maafa za Mkoa huo.

Aidha, mafunzo hayo  ambayo yaliyoandaliwa na Ofisi ya Waziri Mkuu yanatolewa kwa Wajumbe wa Kamati ya Wataalamu ya Usimamizi  wa Maafa, Wajumbe wateule wa Timu ya kukabiliana na Dharura ya Mkoa na wataalamu wa Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura, Waratibu wa Maafa Mkoa na Halmashauri.

Vilevile, Bi. Jane amesema mafunzo hayo yatakuwa mhimili muhimu katika kuhakikisha Mkoa unajiandaa vyema ili kukabiliana na matukio ya dharura kwa haraka hivyo ni lazima timu lengwa ifanye kazi kwa mshikamano ili kuleta ufanisi unaohitajika.

Kwa upande wao  wanufaika wa mafunzo hayo wameishukuru Serikali kwa namna inavyofanya jitihada kuhakikisha wananchi wanaishi katika mazingira salama.

Hivyo, wameahidi kutumia elimu hiyo ya kukabiliana na maafa pindi yanapotokea kuokoa maisha ya watu, mali zao  na kurejesha hali.






Mwanandishi wetu, Morogoro.
WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais, Mhe. Mhandisi Hamad Masauni amesema Usimamizi na uhifadhi wa mazingira hauwezi kufanikiwa kwa kauli au sera peke yake, bali kwa vitendo vinavyoonekana katika ngazi zote ikiwemo shughuli za kupanda miti na kuitunza.

Amesema maono na Matarajio ya Dira 2050 ni makubwa na yanahitaji ubunifu mkubwa katika kufanya kazi ili kufikia matarajio hasa katika mikakati mahsusi ya hifadhi na ustahimilivu wa mabadiliko ya tabianchi.

Waziri Masauni ameyasema hayo Mei 15, 2026 wilayani Kilosa mkoani Morogoro kwenye zoezi la upandaji miti ili kuhakikisha mazingira yanabaki kuwa salama kutokana na uoto wa asili ikiwa moja shughuli zilizopangwa na Ofisi ya Makamu wa Rais kuelekea Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani itakayofanyika Juni 5 mwaka huu ambapo kitaifa itafanyika mkoani Dodoma.

Amesema Dira ya Taifa ya mwaka 2050 ina nguzo kuu tatu na miongoni mwa nguzo hizo ni suala zima la uhifadhi wa mazingira na utahimilivu wa mabadiliko ya tabianchi jambo ambalo kila mmoja anapaswa kulitazama kwa upana wake.

"Haya tunayoyaona hapa kama vile athari za mafuriko, hali ya hewa isiyotabilika inayosababisha ukame na madhara mengine mengi miongoni mwa sababu zake ni mabadiliko ya tabianchi, hivyo kama taifa ni lazima tutoe kipaumbele katika kuhakikisha athari za mabadiliko ya tabianchi tunazihimili," amesema Masuni.

Ameongeza kuwa mtu anaweza asione faida ya upandaji miti lakini ukweli ni kuwa miti hiyo inafaida kuwa katika suala zima la upandaji miti hasa kwa kizazi kichacho cha miaka 50 ijayo kwani ndiyo wenye Tanzania ya baadaye.

Aidha Waziri Masauni aliipongeza Wilaya ya Kilosa na mkoa mzima wa Morogoro kwa kuwahusisha wananafuzi wa shule za msingi na sekondari katika suala zima la upandaji miti na utunzaji mazingira.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Kilosa, Mhe. Shaka Hamdu Shaka kwa niaba ya Mkuu wa mkoa wa Morogoro alisema kuwa wilaya hiyo imejiwekea malengo ya kupanda miti milioni 1.5 na kwamba zoezi hilo limekuwa likifanyika kila mwaka kwa mfululizo wa miaka mitano.

Mhe. Shaka amesema kuwa wilaya yake mara kwa mara imekuwa ikikubwa na mafuriko na kwamba katika kukabiliana na hali hiyo, serikali imedhamilia kujenga mabawa ya maji katika maeneo ya mto Mkondoa ili kuweza kudhibiti mafuriko, hivyo zoezi la upandi miti hiyo kutasaidia kulinda na kufidhi bwawa hilo na hivyo kuchochea maendeleo mbalimbali ya kiuchumi.
Na Mwandishi wetu- MBEYA

Mkurugenzi msaidizi wa Kituo cha Taifa cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Bi. Jane Kikunya amewataka Wajumbe wa Timu ya kukabiliana na Dharura na Uendeshaji wa Kitio cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura ya Mkoa wa Mbeya kufanya kazi kwa ushirikiano, mshikamano na mawasiliano ya karibu ili kutekeleza wajibu wao kwa weledi na ufanisi unaotakiwa.


Mkurugenzi huyo, ameyasema hayo wakati akifungua mafunzo ya siku tano yanayolenga kuziandaa timu za kukabiliana na Maafa za Mkoa huo.

Aidha, mafunzo hayo ambayo yaliyoandaliwa na Ofisi ya Waziri Mkuu yanatolewa kwa Wajumbe wa Kamati ya Wataalamu ya Usimamizi wa Maafa, Wajumbe wateule wa Timu ya kukabiliana na Dharura ya Mkoa na wataalamu wa Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura, Waratibu wa Maafa Mkoa na Halmashauri.

Vilevile, Bi. Jane amesema mafunzo hayo yatakuwa mhimili muhimu katika kuhakikisha Mkoa unajiandaa vyema ili kukabiliana na matukio ya dharura kwa haraka hivyo ni lazima timu lengwa ifanye kazi kwa mshikamano ili kuleta ufanisi unaohitajika.
Kwa upande wao wanufaika wa mafunzo hayo wameishukuru Serikali kwa namna inavyofanya jitihada kuhakikisha wananchi wanaishi katika mazingira salama.

Na Mwandishi Maalum, Mbinga
WAKULIMA na wafanyabiashara wa kahawa wilayani Mbinga,wameishukuru kampuni ya Hagati Company Ltd kuwajengea kiwanda cha kisasa cha kuchakata kahawa Hagati Coffee ambacho kinalenga kuimarisha soko la kahawa na kuondoa changamoto iliyokuwa ikiwakabili wakulima wa zao hilo kwa muda mrefu.

Kiwanda hicho kimewawezesha wakulima na baadhi wafanyabiasha kuanza kuuza kahawa iliyosindikwa kwenye masoko ya ndani na nje ya wilaya ya Mbinga hivyo kuhamasisha unywaji wa kahawa kwa watu ndani na nje ya wilaya ya Mbinga.

Wakizungumza jana kuhusu faida ya kiwanda hicho mkulima wa kahawa wa kijiji cha Kipapa Astel Hili,ameipongeza kampuni hiyo kwa kuwekezakuanzisha kiwanda hicho ambacho kitasaidia kuuza kahawa iliyosindikwa badala ya kuuza kahawa ghafi kwa njia ya mnada ambayo faida yake ni ndogo ikilinganisha na kahawa iliyosindikwa.

“Naimpongeza sana kampuni ya Hagati kutuletea kiwanda hiki cha kisasa,kiukweli kwa sasa tunafanya biashara yetu ya kahawa iliyosindikwa na tunapata wateja wengi wakubwa na wadogo wanaotoka maeneo mbalimbali ya wilaya ya Mbinga na mkoa wa Ruvuma”alisema.

Aidha alisema,kiwanda hicho kimesaidia kutoa ajira kwa baadhi ya wananchi hasa vijana ambao awali hawakuwa na kazi ya kufanya hivyo kujikuta wakidhurura mitaani na wengine kujiingiza kwenye vitendo vya uharifu.

Mfanyabiashara wa kahawa Anold Ndunguru alisema,kuanzishwa kwa kiwanda cha Hagati ni mwanzo mzuri ya safari ya matumaini kwa wadau wengi wa tasinia ya kahawa katika wilaya ya Mbinga ambao sasa watafaidika na zao hilo na kupunguza vitendo vya ununuzi wa kahawa ghafi kwa njia haramu ya magoma.

Mmiliki wa kiwanda hicho Abubakari Ali Abubakar alisema,mkakati wa Hagati Company Ltd kupitia bidhaa zake za Hagati Coffee ni kusogeza huduma bora na kuunga mkono mkakati wa Serikali wa kuhamasisha jamii kupenda kunywa kahawa yenye umuhimu mkubwa kwa afya ya binadamu.

Abubakari,alisema kunywa kahawa kuna faida nyingi ikiwemo kuongeza kinga dhidi ya ugonjwa wa ini,inapunguza uwezekano wa kupata magonjwa ya akili na kisukari.

Alisema,Hagati Company Ltd inatambua changamoto ya kipato kwa Watanzania wengi,hivyo inachakata na kuuza bidhaa za kahawa kuanzia gramu 50,100,200 na kilo moja ili kuhakikisha huduma hiyo inapatikana kwa gharama nafuu zaidi.

Alisema,Hagati Company Ltd itaendelea kuimarisha ushindani katika huduma zake za Hagati coffee ili kuhamasisha wananchi hata wa kipato cha chini kupenda kunywa kahawa na kuwapunguzia gharama katika matumizi ya kila siku.

Ametaja maduka yanayouza bidhaa za Hagati coffee kwa upande wa Mbinga ni Erick Shop karibu na benki ya NMB,Kilocha Shop,Songea dukani kwa Kaburu jirani na soko kuu la manispaa ya Songea na Dar es slaam duka lipo Kigamboni njia panda ya kwenda Kisota.

“wenyeji wa mkoa wa Ruvuma wanalima sana kahawa lakini suala la unywaji ni changamoto kubwa,wanywaji wakubwa wa kahawa hawapo hapa Mbinga wapo nje ya nchi na ndiyo wanaojua thamani ya kahawa hii”alisema.

Alisema,yeye ni mzaliwa wa Mbinga hivyo ameona jina sahihi la kuipandisha hadhi kahawa inayolimwa Mbinga ni jina la Hagati coffee ambalo ni bonde maarufu kwa uzalishaji wa kahawa safi inayosifika ulimwenguni kote.

Amewaomba wakulima kupitia vyama vyao vya msingi vya ushirika(Amcos)wafanyabiashara na wadau wa tasinia ya kahawa kutumikia kiwanda cha Hagati coffee kwa usindikaji ili waweze kupata kahawa bora itakayokubali kwenye soko la ndani na nje ya nchi.

Na Oscar Assenga Tanga
JUKWAA la Wanawake na Kodi limefanyika leo Jijini Tanga huku ikielezwa ni hatua muhimu inayodhihirisha dhamira ya kuendeleza usawa wa kijinsia na kukuza uchumi shirikishi nchini.

Akizungumza wakati akifungua Jukwaa hilo Meneja wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Tanga, CPA Castro John, alisema ni dhamira ya dhati ya kujenga mfumo wa kodi unaoshirikisha makundi yote ya jamii, hususan wanawake ambao ni nguzo muhimu ya uchumi wa Taifa.


Alisema takwimu zinaonesha wanawake wanachangia kwa kiwango kikubwa katika shughuli mbalimbali za kiuchumi zikiwemo biashara ndogondogo, kilimo, huduma, viwanda vidogo pamoja na biashara za kati na kubwa.

Kwa mujibu wa takwimu za mwaka 2024/2025, wanawake nchini, wakiwemo wa Mkoa wa Tanga, wanakadiriwa kushiriki katika nguvu kazi kwa asilimia 80, huku wakimiliki asilimia 54 ya biashara ndogo, za kati na kubwa.

“Bila ushiriki wa wanawake, juhudi za kuongeza wigo wa walipa kodi na kuongeza mapato ya ndani haziwezi kufikia malengo yaliyokusudiwa,” alisema CPA Castro John.


Alifafanua kuwa TRA imeanzisha Jukwaa hilo maalumu kwa lengo la kutoa elimu sahihi ya kodi, kusikiliza changamoto za wanawake wafanyabiashara, kujenga ushirikiano wa karibu pamoja na kuhamasisha ulipaji wa kodi kwa hiari na kwa wakati.

Aidha, alisema TRA imejikita katika kuboresha huduma kwa kuzingatia ushirikishwaji, uwazi, weledi na urahisi wa upatikanaji wa huduma. Aliongeza kuwa elimu ya kodi na mahusiano bora ni msingi muhimu wa kuongeza utii wa kodi.

Kupitia jukwaa hilo, wanawake watapata nafasi ya kupata ushauri kuhusu masuala ya kodi, kujifunza fursa mbalimbali pamoja na kuelewa wajibu wao wa kikodi.


“Tunataka mwanamke ajisikie salama, aheshimiwe na ashiriki kikamilifu katika mfumo wa kodi bila hofu wala kikwazo chochote,” alisema.

CPA Castro John alisisitiza kuwa kodi ndiyo injini ya maendeleo ya Taifa kwani mapato yake yanagharamia huduma muhimu kama elimu, afya, barabara, maji safi na miradi mingine ya kimkakati.

“Kila mwanamke anayelipa kodi anakuwa mshirika wa moja kwa moja wa Serikali katika kujenga Tanzania yenye uchumi imara na huduma bora kwa wananchi wake,” aliongeza.

Pia aliwataka wanawake kutumia jukwaa hilo kujifunza, kuuliza maswali na kuwa mabalozi wa utamaduni wa kulipa kodi katika jamii zao.


Aidha, aliwataka wadau wa sekta mbalimbali pamoja na taasisi za kifedha kuendelea kushirikiana na TRA katika kuwawezesha wanawake kukuza biashara zao kwa kuzingatia misingi ya kikodi.

Kwa upande mwingine, aliwahimiza wanawake wafanyabiashara kujisajili katika mfumo wa kodi na kutekeleza wajibu wao kwa hiari na kwa wakati.


“Kulipa kodi si wajibu wa kisheria tu, bali ni mchango wa moja kwa moja katika kujenga Taifa. Wanawake wakisimama kiuchumi, familia na jamii vinaimarika,” alisema.

Katika hatua nyingine, alisisitiza umuhimu wa kutumia mipaka rasmi ya biashara kwa wafanyabiashara wanaovuka mipaka kupitia maeneo ya Horohoro na Pangani, huku akiwataka kuachana na biashara za magendo na matumizi ya njia zisizo rasmi.


Naye Naibu Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Wafanyabiashara nchini, JW Ismail Masound, alisema jukwaa hilo lina umuhimu mkubwa kutokana na malengo ya Dira ya Taifa ya mwaka 2050 ambapo sekta binafsi inatarajiwa kuwa mhimili mkubwa wa ukuaji wa uchumi.

Alisema majukwaa hayo yanasaidia kuwawezesha wanawake na wafanyabiashara kufikia malengo ya maendeleo ya Taifa kwa kuongeza ushiriki wao katika shughuli za kiuchumi.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Jukwaa la Wanawake Mkoa wa Tanga (TWCC), Aziza Ramadhani, alisema jukwaa hilo litawasaidia wanawake kuelewa umuhimu wa kulipa kodi katika kukuza uchumi wa Mkoa wa Tanga na Taifa kwa ujumla.

“Hivyo ni wajibu wetu kuhakikisha Mkoa wa Tanga unalipa kodi kutokana na umuhimu wake kwa maendeleo ya jamii,” alisema.

Aliongeza kuwa jukumu la jukwaa hilo ni kuwaunganisha wanawake wa Mkoa wa Tanga ili kuwapa nafasi ya kujifunza, kushirikiana na kupata fursa mbalimbali za kiuchumi ndani na nje ya mkoa huo.

Aidha, alisema wamekuwa wakitoa mafunzo mbalimbali ikiwemo kuanzisha mashamba darasa kwa vijana wa kiume na wa kike, huku akiwakaribisha wanawake wajasiriamali kushiriki katika shughuli za maendeleo zinazochangia ukuaji wa uchumi wa Mkoa wa Tanga na Taifa kwa ujumla.

Na Mwandishi Wetu
MWENYEKI wa Chama cha mawakili wa Serikali, Addo November amesema mbio za Wakili Marathon zitakazofanyika Mei 31 mwaka huu mjini Dodoma zinalenga kuhamasisha utoaji wa msaada wa kisheria pamoja na kuwajengea Watanzania utamaduni wa kufanya mazoezi kwa ajili ya afya zao.

Akizungumza na waandishi wa habari Mei 17,2026 Jijini Dar es salaam, November amesema mbio hizo zitawakutanisha viongozi wa serikali, mawakili, wanamichezo na wananchi wa kawaida katika kuunga mkono kampeni ya msaada wa kisheria inayotekelezwa chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan kupitia Samia Legal Aid Campaign.

Amesema hadi sasa mamilioni ya Watanzania tayari wamefikiwa na huduma za msaada wa kisheria bure, huku changamoto kubwa zinazowakabili wananchi wengi zikiwa ni migogoro ya ardhi, ndoa pamoja na unyanyasaji wa aina mbalimbali, jambo lililoifanya jamii kuendelea kuhitaji msaada huo muhimu.

November ameeleza kuwa marathon hiyo itakuwa na mbio za kilomita 21 pamoja na mbio za umbali mfupi kwa washiriki wa rika tofauti, huku watoto nao wakitengewa nafasi maalumu ya kushiriki ili kukuza vipaji vya michezo tangu wakiwa wadogo.

Aidha amesema maandalizi yote muhimu yamekamilika ikiwemo uwepo wa huduma za afya kutoka Shirika la Red Cross, vituo vya maji na matunda kwa washiriki pamoja na utoaji wa medali na zawadi kwa washindi wa mashindano hayo.

Aidha November amesema washiriki watatakiwa kulipia Sh40,000 kwa ajili ya usajili ambapo watapatiwa vifaa mbalimbali vya marathon hiyo, huku akibainisha kuwa lengo la awali ni kupata washiriki zaidi ya 5,000 kutoka maeneo mbalimbali nchini.

Ameongeza kuwa mbio hizo zitapambwa na burudani kutoka kwa wasanii mbalimbali pamoja na uwepo wa viongozi wa kitaifa akiwemo Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Hamza Johari huku majina mengine ya wageni maalumu yakiendelea kutangazwa kadri siku zinavyosogea.

Naye mwanariadha mstaafu, Juma Ikangaa amesema marathon hiyo itasaidia kuibua vipaji vipya vya riadha nchini na kuongeza hamasa ya Watanzania kushiriki michezo kwa manufaa ya afya na maendeleo ya taifa.

Amesema ushiriki wa wanasheria katika mbio hizo unaonyesha namna taaluma hiyo ilivyo tayari kushirikiana na jamii katika shughuli za maendeleo, huku akiwataka Watanzania kujitokeza kwa wingi kushiriki tukio hilo la kihistoria litakalofanyika katika Viwanja vya Jamhuri mkoani Dodoma.


 Na Mwandishi Wetu, Arusha

Arusha. Tarehe 15 Mei 2026: Serikali imeipongeza Benki ya CRDB Bank Plc kwa juhudi zake za kuhamasisha uwekezaji nchini kupitia elimu ya fedha, uwekezaji wa hisa na uwezeshaji wa kiuchumi unaolenga kuwajenga vijana kuwa wawekezaji wa baadaye.

Pongezi hizo zimetolewa jana jijini Arusha na Waziri wa Fedha, Khamis Mussa Omar wakati akifungua Semina ya Wanahisa wa Benki ya CRDB iliyofanyika sambamba na Mkutano Mkuu wa 31 wa mwaka wa benki hiyo katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC).

Semina hiyo ilikuwa na kaulimbiu isemayo “Vijana na Uwekezaji kwenye Hisa” na iliwakutanisha viongozi wa serikali, wanahisa, wataalamu wa masoko ya mitaji pamoja na vijana kutoka maeneo mbalimbali nchini.

Akizungumza katika semina hiyo, Waziri Omar alisema vijana wanapaswa kushiriki kikamilifu katika umiliki wa uchumi kupitia uwekezaji badala ya kutegemea ajira pekee.

“Kaulimbiu ya mwaka huu imebeba ujumbe mkubwa wa kimkakati kwa taifa letu. Vijana hawapaswi kuishia kutafuta ajira pekee, bali wanastahili kushiriki katika umiliki wa uchumi kupitia uwekezaji,” alisema Waziri Omar.

Aidha, aliipongeza benki hiyo kwa hatua ya kufungua Ofisi ya Uwakilishi Dubai, akisema hatua hiyo imeongeza hadhi ya Tanzania katika sekta ya fedha na uwekezaji kimataifa.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela alisema benki hiyo itaendelea kuwawezesha vijana kupitia huduma za kifedha, ubunifu na programu za maendeleo ya ujasiriamali.

Alisema kupitia CRDB Bank Foundation na programu ya IMBEJU, maelfu ya vijana na wafanyabiashara wadogo wamefikiwa kwa mafunzo, mitaji na ushauri wa biashara.

“Tunaamini vijana wa leo si wateja tu wa benki yetu, bali ni wawekezaji, wabunifu na viongozi wa uchumi wa kesho,” alisema Dkt. Nsekela.

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Benki ya CRDB, Neema Mori alisema uwekezaji katika hisa ni njia muhimu ya kujenga ustawi wa kifedha wa muda mrefu kwa vijana na familia za Kitanzania.

Profesa Mori alisema mafanikio ya Benki ya CRDB yanaonyesha namna uwekezaji wa muda mrefu unavyoweza kuleta matokeo chanya kwa wanahisa.

Alibainisha kuwa ndani ya miaka mitatu iliyopita thamani ya hisa za benki hiyo imeongezeka kwa zaidi ya asilimia 253, huku bei ya hisa ikifikia wastani wa Sh2,800 kutoka Sh460 mwaka 2023.

Aidha, alisema bodi ya wakurugenzi inapendekeza gawio la Sh90 kwa kila hisa kutokana na matokeo mazuri ya kifedha ya mwaka 2025, ikiwa ni ongezeko la asilimia 38 ikilinganishwa na mwaka uliopita.

Profesa Mori aliwahamasisha wazazi kuanza kuwawekezea watoto wao hisa mapema ili kuwajengea msingi imara wa maisha ya kifedha ya baadaye.

Benki ya CRDB ni miongoni mwa taasisi kubwa za kifedha Afrika Mashariki na Kati, ikiwa na zaidi ya wateja milioni sita katika nchi za Tanzania, Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo pamoja na ofisi ya uwakilishi Dubai, Falme za Kiarabu.




 Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akizungumza wakati akifungua Semina ya Wanahisa wa Benki ya CRDB katika Mkutano Mkuu wa 31 wa Wanahisa, uliobeba kauli mbiu ya “Vijana na Uwekezaji kwenye Hisa”, semina inayofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC), ambapo alitoa wito kwa Taasisi za Fedha nchini kupunguza riba na gharama nyingine za mikopo ili kuwawezesha wananchi wakiwemo vijana kupata mitaji ya kuwekeza kwenye shughuli zao za kiuchumi.

 Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Dkt. Abdulmajid Nsekela, akizungumza wakati wa hafla ya ufunguzi wa Semina ya Wanahisa wa Benki ya CRDB katika Mkutano Mkuu wa 31 wa Wanahisa hao, uliobeba kauli mbiu ya “Vijana na Uwekezaji kwenye Hisa”, uliofunguliwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (hayupo pichani), uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC).

 Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Benki ya CRDB, Prof. Neema Mori, akizungumza wakati wa hafla ya ufunguzi wa Semina ya Wanahisa wa Benki ya CRDB katika Mkutano Mkuu wa 31 wa Wanahisa hao, uliobeba kauli mbiu ya “Vijana na Uwekezaji kwenye Hisa”, uliofunguliwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (hayupo pichani), uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC).







































Top News