Serikali ya Tanzania imeingia makubaliano na kampuni mbili kutoka Japan kwa ajili ya kufungua fursa za soko la biashara ya kaboni kupitia mpango wa Uratibu wa Pamoja wa Mikopo (JCM), hatua inayolenga kuongeza mchango wa sekta binafsi katika kufanikisha dira ya taifa ya maendeleo ya mwaka 2050.

Akizungumza katika warsha ya kusaini Hati ya makubaliano hayo, Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, Dkt. Richard Mayungi, alisema serikali ina jukumu la kuhakikisha dira ya 2050 inafikiwa kupitia uwekezaji katika nishati safi, biashara ya kaboni na udhibiti wa taka.

Kwa upande wake, Afisa Mtendaji Mkuu wa Kituo cha Biashara ya Kaboni (NCMC), Ngenda Kigaraba, alibainisha kuwa utoaji wa mikopo kwa pamoja utasaidia kulinda mazingira, kukuza biashara na kuongeza mapato ya Serikali.

Naye Afisa Mtendaji Mkuu wa kampuni ya 3T kutoka Japan, Kan Shimizu, alisema Tanzania itanufaika kwa kiasi kikubwa kupitia ushirikiano huu, hususani katika sekta ya utunzaji wa mazingira na biashara ya kaboni

Makubaliano haya ya ushirikiano kati ya NCMC na kampuni za Japan yanalenga kuchochea mchango wa sekta binafsi katika kufanikisha malengo ya Dira ya taifa ya mwaka 2050, ambapo nguzo ya tatu ya Dira hiyo inasisitiza ukuaji wa uchumi wa Taifa na maendeleo endelevu yanayozingatia mazingira endelevu.

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali itaendelea kulinda amani, usalama wa wananchi na rasilimali za Taifa na haitamvumilia mtu yeyote atakayejihusisha na vitendo vinavyohatarisha usalama wa nchi.

Ametoa kauli hiyo leo (Jumamosi, Juni 27, 2026) alipowasalimia wananchi wa Wilaya ya Ikungi, mkoani Singida, ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya kikazi mkoani humo.

Waziri Mkuu amesema Serikali imeendelea kufuatilia taarifa kuhusu watu wanaodaiwa kupanga au kufadhili vitendo vinavyoweza kuvuruga amani ya nchi na kwamba vyombo vya ulinzi na usalama vitaendelea kuchukua hatua kwa mujibu wa sheria dhidi ya wote watakaobainika kujihusisha na vitendo hivyo.

"Hatutafanya mzaha na mtu wa aina hiyo. Tumepewa jukumu la kuilinda nchi yetu na watu wake, na hatutafanya mchezo kwenye jambo hilo."

Amesema Serikali haina mgogoro na chama chochote cha siasa kwa kuwa vyama hivyo vinatambuliwa na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, bali itaendelea kutekeleza wajibu wake wa kulinda amani, usalama wa Taifa na wananchi wake wakati wote.

"Hatuna ugomvi na chama chochote cha siasa. Lakini tuna jambo ambalo ni kipaumbele, usalama wa Tanzania na usalama wa Watanzania."

Aidha, Waziri Mkuu amewataka wananchi kuendelea kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama kwa kutoa taarifa za vitendo vinavyoweza kuhatarisha amani na kuendelea na shughuli zao za uzalishaji bila hofu.

Pia amesema Serikali itaendelea kutekeleza miradi ya maendeleo katika Mkoa wa Singida ikiwemo ujenzi na uboreshaji wa barabara, reli ya kisasa (SGR), uwanja wa ndege pamoja na miradi ya maji, afya na elimu kwa lengo la kuboresha huduma za wananchi na kuchochea maendeleo ya uchumi.

Kwa upande wake, Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Dkt. Jafar Seif amesema Serikali itaendelea kushirikiana na viongozi wa Mkoa wa Singida kuhakikisha fedha za maendeleo zinaelekezwa katika utekelezaji wa miradi yenye tija kwa wananchi, huku mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na halmashauri ikiendelea kuwafikia walengwa kwa wakati.






Na MWANDISHI WETU

Dar es Salaam. Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu, amewaaga vijana 400 wa Kitanzania wanaokwenda kufanya kazi nje ya nchi, akisisitiza umuhimu wa kujiunga na Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) na kuchangia katika Mfuko huo ili kujihakikishia ulinzi wa kijamii na ustawi wa maisha yao ya sasa na baadaye.

Alisema hayo jijini Dar es Salaam wakati wa hafla ya kuwaaga vijana hao, ambao pia walipata elimu ya hifadhi ya jamii kutoka NSSF ikiwa ni sehemu ya kuwaandaa kwa maisha na ajira zao nje ya nchi.

Akizungumza katika hafla hiyo, Waziri Sangu alimpongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uongozi wake imara unaoendelea kuimarisha diplomasia ya ajira na kufungua fursa salama kwa Watanzania kufanya kazi nje ya nchi, hatua inayoongeza usalama na heshima ya wafanyakazi wa Kitanzania katika soko la ajira la Kimataifa.

Aidha, alisema Serikali inaendelea kupanua wigo wa hifadhi ya jamii ili kuwafikia Watanzania wengi zaidi, hususan vijana na wananchi waliojiajiri, akieleza kuwa Hifadhi Skimu imekuwa nyenzo muhimu ya kuwaunganisha wananchi na mfumo wa hifadhi ya jamii.

“Nitumie fursa hii kuipongeza Benki ya CRDB na NSSF.Hii ni kazi ya kimkakati kwa mustakabali wa vijana wetu. Zamani walikuwa wakiondoka bila uelewa wa hifadhi ya jamii, lakini sasa kupitia Hifadhi Skimu wanapata elimu na kuelezwa faida za kujiunga na kuchangia, ikiwemo kunufaika na mafao mbalimbali yakiwemo ya matibabu kwao na familia zao,” alisema Waziri Sangu.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa NSSF, Bw. Masha Mshomba, alimshukuru Waziri Sangu kwa kuendelea kuipa kipaumbele sekta ya hifadhi ya jamii katika ajenda ya kazi zenye staha, sambamba na kumpongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kufungua fursa za ajira ndani na nje ya nchi kwa Watanzania.

Alisema NSSF inaendelea kuboresha huduma zake kupitia mafao mbalimbali, yakiwemo pensheni ya uzee, urithi, ulemavu, uzazi, upotevu wa ajira pamoja na matibabu, akisisitiza kuwa lengo ni kuhakikisha kila mwanachama analindwa katika kila hatua ya maisha yake.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Huduma za Ajira Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Ajira na Mahusiano Bi. Jane Sorogo, alimshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uongozi wake unaoendelea kupanua fursa za ajira nje ya nchi kwa Watanzania, pamoja na Waziri Sangu kwa kuhakikisha wanaokwenda kufanya kazi nje ya nchi wanafuata taratibu sahihi na haki zao zinalindwa.

Alibainisha kuwa mafanikio ya ajira za nje yanategemea ushirikiano kati ya Serikali, taasisi za umma na sekta binafsi. Aidha, alizishukuru Benki ya CRDB na NSSF kwa kutoa elimu ya hifadhi ya jamii na kuwaandikisha vijana hao katika Hifadhi Skimu ili waanze kujiwekea akiba na kunufaika na mafao yanayotolewa na Mfuko.


















Na Mwandishi Wetu.

KAMPUNI ya Oryx Gas Tanzania kwa kushirikana na taasisi ya Kidoti Foundation wameingia makubaliano ya kuendelea kuhamasisha matumizi ya nishati safi nchini kwa kulifiki kundi la watoa huduma za Saluni nchini.

Kwa mujibu wa Oryx na Kidodi Foundation watoa huduma za Saluni nchini ni kundi lenye uwezo mkubwa wa kuharakisha matumizi ya nishati safi ya kupikia kutokana na mwingiliano wao wa karibu na jamii, hali inayowafanya kuwa mabalozi muhimu wa mabadiliko ya tabia na mtazamo kuhusu matumizi ya nishati hiyo.

Akizungumza Jijini Dar es Salaam wakakati wa hafla ya kusaini makubaliano hayo Mkurugenzi wa Kidoti Foundation, Jokate Mwegelo, ambaye pia ni mlezi wa Chama cha Salunisti Tanzania (CCST) amesema lengo la kuwawezesha watoa huduma za saluni kutumia nishati safi na kuwa mabalozi wa kuhamasisha matumizi yake katika jamii.

Amesema kundi la wasusi na watoa huduma za saluni lina nafasi ya kipekee kwa kuwa hukutana na mamia ya wananchi kila siku, jambo linaloweza kutumiwa kueneza elimu kuhusu manufaa ya nishati safi ya kupikia kwa urahisi kuliko kutegemea kampeni za kawaida pekee.

Amefafanua watoa huduma za saluni wanazungumza na watu wa makundi mbalimbali kila siku. Wanajenga mahusiano ya karibu na wateja wao, hivyo wana nafasi kubwa ya kubadilisha mitazamo kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia.

“Tunataka wawe mabalozi wa mabadiliko hayo na kupitia makubaliano haya tumeyaingia Kati ya Kidoti Foundation na Oryx Gas Tanzania matarajio yetu tutawafikia watoa huduma wote wa saluni kupitia chama chao ambapo tutawapatia mitungi ya gesi na tutaanza na mitungi 2000 ambayo itatolewa kwa awamu.

Juhudi za kuhakikisha Watanzania wengi wanatumia nishati safi haziwezi kuachiwa Serikali pekee, bali zinahitaji ushiriki wa makundi yenye ushawishi wa moja kwa moja katika jamii.

Kundi la watoa huduma za saluni limesahaulika kwa muda mrefu lakini Kidoti Foundation tumeona iko haja ya kulishika kundi hili kwa kuliwezesha kutumia nishati safi ya kupikia.”

Jokate amesema saluni zimekuwa sehemu ambazo mbali na huduma za urembo, wananchi hubadilishana uzoefu kuhusu afya, biashara, malezi na masuala mbalimbali ya maendeleo, hivyo zinaweza pia kuwa majukwaa ya utoaji wa elimu kuhusu nishati safi.

Pia amesema kupitia ushirikiano huo, watoa huduma za saluni watanufaika kwa kutumia nishati safi katika shughuli zao za kila siku, huku wakipata nafasi ya kuwahamasisha wateja wao kuachana na matumizi ya nishati zinazochafua mazingira na kuhatarisha afya.

"Nishati safi si suala la kupikia pekee. Ni suala la afya, mazingira, uchumi wa familia na maendeleo ya taifa. Tukiwafikia wasusi, tutakuwa tumefikia maelfu ya familia kupitia wateja wao," amesema.

Kwa upande wake Meneja Mauzo wa Oryx Tanzania Shaban Fundi amesema kampuni hiyo imeamua kushirikiana na Kidoti Foundation kwa kutambua kuwa makundi ya kijamii yenye ushawishi yanaweza kuongeza kasi ya matumizi ya nishati safi nchini.

“Mbali na kutoa suluhisho la nishati safi, kampuni yetu itaendelea kujenga uelewa wa wananchi kuhusu faida za matumizi ya gesi na teknolojia nyingine za kisasa zinazochangia kulinda afya na mazingira,”amesema na kusisitiza Oryx Gas na Kidoti Foundation kupitia makubaliano yanakwenda kuongeza watumiaji wa nishati safi nchini.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa CCST Ntuli Mwakatobe amesema amesema ushirikiano huo ni hatua muhimu ya kuwawezesha wanachama wa chama hicho kuwa sehemu ya utekelezaji wa ajenda ya nishati safi nchini.

Amesema wasusi na wamiliki wa saluni wamekuwa wakitafuta njia za kupunguza gharama za uendeshaji wa biashara zao huku wakihakikisha mazingira ya kazi yanakuwa salama zaidi.

"Leo tunapata nafasi ya kutumia nishati safi lakini pia kuwa sauti ya kuelimisha jamii. Hii ni fursa ambayo tutaenda kuitumia kuwafikia wateja wetu kila siku," amesema.

Matumizi ya nishati safi ya kupikia yanatajwa kuchangia kupunguza uzalishaji wa hewa ukaa unaochochea mabadiliko ya tabianchi, sambamba na kuboresha maisha ya wanawake ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakibeba mzigo mkubwa wa shughuli za kupikia.





Na Seif Mangwangi, Michuzi TV, Arusha


VIJANA zaidi ya 77, 000 kutoka mikoa nane wanaojishughulisha na ujasiriamali wa kilimo na ufugaji nchini, wamepatiwa mafunzo ya matumizi sahihi ya fedha Ili kuwasaidia kuboresha shughuli zao na jamii inayowazunguka.

Mafunzo hayo ambayo yametolewa na chuo cha Benki Kuu ya Tanzania (BOT), kwa ufadhili wa mfuko wa chakula Duniani (WFP), vijana hao wametoka katika mikoa ya Arusha, Manyara, Morogoro, Dodoma, Shinyanga, Simiyu, Tabora na Singida.

Akizungumza wakati wa kufunga mahafali ya kuhitimu mafunzo hayo kwa vijana kutoka mikoa mitano ya Morogoro, Arusha, Singida, Dodoma na Manyara , Mkuu wa chuo cha benki Kuu Tanzania, Dk.Nicas Yuna amesema elimu waliyopewa vijana hao ni silaha ya kuwakwamua kiuchumi.

Amesema vijana hao wanatakiwa kutumia elimu waliyoipata kupitia mafunzo hayo kuwafundisha vijana wengine na kwamba chuo cha benki kuu kitafuatilia kujua matokeo ya mafunzo hayo kwa Kila kijana aliyehudhuria.

“ Haya ni mafunzo ambayo yanatakiwa kusambaa zaidi, na hawa ni vijana wachache walioteuliwa Ili waweze kwenda kuwa walimu Kwa vijana wengine, tunaamini wakiisambaza elimu hii vizuri, vijana wengi watafaidika na kujikwamua kiuchumi,” amesema Dkt Yuna.

Amesema katika mafunzo hayo ambapo pia walialikwa wakufunzi kutoka taasisi za benki ili kutoa elimu ya namna ya kukopa, bima kwaajili ya usalama wa mazao na mifugo pamoja na mfuko wa uwekezaji UTT, walifundishwa masomo ya namna ya kutafuta fedha halali, kubana na kutunza fedha kwaajili ya uwekezaji.

Afisa habari wa WFP nchini, Brigitha Lyimo amesema mafunzo hayo ni muendelezo wa mradi wa miaka mitano wa vijana kilimo Biashara kwaajili ya kuwawezesha vijana katika ujasiriamali wa kilimo ulioanza mwaka 2023.

Kaimu Mkurugenzi wa WFP nchini Tanzania, Christine Mendes amelishukuru shirika la Mastercard foundation Kwa ufadhili wa programu hiyo ya kumwezesha kijana na kusema ni matarajio ya WFP kuwa wahitimu wa mafunzo hayo wataenda kuibadilisha jamii wanayotoka kwa kuendeleza kilimo na ufugaji kwa kutumia mbinu za kisasa za matumizi sahihi ya fedha.

“ Kwa msaada wa mfuko wa wakfu wa Mastercard, WFP inatekeleza programu ya Vijana Kilimo Biashara (VKB), Ili kuunda na kutengeneza fursa za kazi zenye heshima na utiifu Kwa vijana kupitia mnyororo wa thamani ya kilimo,pia programu hii inatambua kuwa uwezo wa kifedha ni muhimu kwa ujasiriamali, ukuaji wa biashara na mabadiliko ya muda mrefu ya kiuchumi,” Amesema.

Amesema katika mahafali hayo ambapo jumla ya wahitimu walimu wa fedha 79 walihitimu na kukabidhiwa vyeti, kunakamilisha idadi ya wahitimu 150 kufuatia vijana wengine71 kuhitimu mafunzo ya aina hiyo hiyo Jijini Mwanza na kwamba Mtandao huo unaokua unawakilisha uwekezaji muhimu Kwa watu na taasisi ambao utaendelea kuimarisha ushirikishwaji wa fedha Tanzania nzima.

Amesema mafunzo hayo yatawasaidia vijana kukuza ujasiri wa kuweka akiba, kuwekeza, kuweka rekodi, kupata huduma za kifedha na kufanya maamizi sahihi ya kibiashara.








Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB), Bw. Asangye Bangu, amesema Bodi inatarajia kuongeza bidhaa nyingine tano katika Mfumo wa Stakabadhi za Ghala ili kuendelea kuwanufaisha watanzania katika sekta mbalimbali.

Akifungua kikao cha wadau cha kujadili na kupitisha Rasimu ya Mpango Mkakati wa WRRB wa miaka mitano (2026/27–2030/31) pamoja na kupokea maoni kuhusu maboresho ya Kanuni za Stakabadhi za Ghala, kilichofanyika Juni 26, 2026, mjini Morogoro, Bw. Bangu amesema mfumo huo umeendelea kukua kwa kasi na kuleta mafanikio makubwa.

Amesema katika kipindi cha miaka mitano iliyopita mfumo huo ulikuwa unahusisha bidhaa mbili pekee, lakini kwa sasa unahusisha bidhaa 18, huku maandalizi yakiendelea kuongeza bidhaa nyingine tano ili kuimarisha uwazi, ushindani wa bei na kuongeza fursa za biashara ya mazao.

Bw. Bangu amebainisha kuwa pamoja na kuwanufaisha wakulima kwa kuwawezesha kuuza mazao yao kwa bei yenye ushindani, mfumo huo umechangia kuongeza mapato ya Serikali na kurahisisha Halmashauri kukusanya mapato yatokanayo na biashara ya mazao.

Aidha, amesema WRRB inaendelea na mazungumzo na Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) pamoja na Bodi ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko (CPB) ili kuwezesha biashara ya mazao kufanyika kupitia Mfumo wa Stakabadhi za Ghala, hatua itakayoongeza ufanisi na uwazi katika biashara hiyo.

Ameongeza kuwa Bodi itaendelea kuhamasisha matumizi ya mfumo huo kwa kuanzisha njia bunifu zitakazowasaidia wakulima kuepuka kuuza mazao yao mara tu baada ya mavuno, wakati bei zikiwa chini.

Top News