Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma .

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amesema vijana ndio nguzo kuu ya uendeshaji wa Serikali ya awamu ya sita, akisisitiza kuwa mustakabali wa taifa uko mikononi mwao kutokana na idadi yao kubwa nchini.

Akizungumza katika Kongamano la Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi lililofanyika Tunguu, Zanzibar, Rais Samia alisema takwimu za Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2022 zinaonyesha wazi kuwa vijana ndio kundi kubwa la Watanzania, hivyo wanapaswa kupewa nafasi pana zaidi katika maamuzi ya maendeleo ya taifa.

Amefafanua kuwa Serikali imeweka mikakati madhubuti ya kuboresha mazingira ya kiuchumi, kijamii na kisiasa ili kuwawezesha vijana kushiriki kikamilifu katika uongozi na kujenga taifa lenye ushindani.

“Serikali hii inaendeshwa na vijana. Sisi tuliopo juu kazi yetu ni kutoa mwelekeo, kusimamia sera na kurekebisha mifumo ya kisheria pale inapohitajika,” alisema Rais Samia.

Aidha, amebainisha kuwa muundo wa sasa wa Serikali unaonesha dhamira hiyo, ambapo idadi kubwa ya mawaziri na manaibu mawaziri ni vijana. Aliongeza kuwa hata katika vikao vya Baraza la Mawaziri, zaidi ya robo tatu ya wajumbe waliohudhuria walikuwa chini ya umri wa miaka 50.

Rais Samia amesisitiza kuwa hatua hiyo si ya bahati mbaya, bali ni utekelezaji wa dira ya maendeleo ya taifa pamoja na maelekezo ya Ilani ya Chama Cha Mapinduzi, ambayo inaelekeza kuwekeza nguvu zaidi kwa vijana.

Kwa upande mwingine, aliwataka vijana kote nchini kutumia fursa wanazopewa kwa uwajibikaji, nidhamu na uzalendo, ili kuhakikisha wanachangia kikamilifu katika kukuza uchumi na ustawi wa jamii.












Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Jabir Shekimweri, amesisitiza kuwa uendelevu wa Taifa hauwezi kupatikana iwapo wananchi hawatazingatia utunzaji wa mazingira, akieleza kuwa changamoto za mabadiliko ya tabia nchi zinaweza kuathiri ustawi wa jamii na maendeleo ya nchi kwa ujumla.

Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule, katika maadhimisho ya miaka 62 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar yaliyofanyika kimkoa katika viwanja vya Shule ya Msingi NaneNane, kata ya Nzuguni, Shekimweri amesema ni muhimu kwa wananchi kushiriki kikamilifu katika kulinda mazingira ili kukabiliana na athari kama ukame.

Katika kuadhimisha Muungano huo, Shekimweri alishiriki zoezi la upandaji miti katika Shule ya Msingi NaneNane, ambapo jumla ya miti 162 imepandwa, ameeleza kuwa idadi hiyo inaashiria miaka ya Muungano na umoja wa Taifa, Aidha, amewataka wanafunzi na walimu kuitunza miti hiyo ili iweze kukua na kuleta manufaa kwa kizazi cha sasa na kijacho.

Sambamba na hilo, amewataka wananchi kuendelea kuuenzi Muungano wa Tanganyika na Zanzibar kwa kudumisha amani, umoja na mshikamano ulioasisiwa na waasisi wa Taifa la Tanzania, Amesema misingi hiyo inapaswa kuanzia kwa mtu mmoja mmoja, familia, jamii hadi Taifa kwa ujumla.

Aidha, amebainisha kuwa katika kipindi cha miaka 62 ya Muungano, nchi imepiga hatua kubwa katika sekta mbalimbali ikiwemo afya na usafirishaji. Amesema huduma za afya sasa zinapatikana hadi ngazi ya kata kutokana na upatikanaji wa vifaa tiba, hali iliyopunguza adha ya wananchi kusafiri umbali mrefu kufuata matibabu.

Kwa upande wa usafirishaji, amesema maboresho yaliyofanyika yamerahisisha safari, ambapo kwa sasa inawezekana kusafiri kutoka Dodoma kwenda Zanzibar na kurejea siku hiyo hiyo, tofauti na ilivyokuwa hapo awali.

Maadhimisho ya miaka 62 ya Muungano yalianza Aprili 24, 2026 kwa shughuli mbalimbali ikiwemo usafi kwenye kata zote, mdahalo, maandamano ya amani ya kilomita 6.2 na bonanza la michezo, kabla ya kuhitimishwa Aprili 26, 2026 kwa zoezi la upandaji miti.




Na Said Mwishehe,Michuzi TV-Manyoni

HOSPITALI ya Wilaya ya Manyoni mkoani Singida imesema hospitali hiyo kwa sasa imekuwa na uwezo mkubwa wa utoaji bora wa huduma za afya kutokana na uwepo wa dawa na vifaa tiba vya kisasa vilivyotolewa na Bohari ya Dawa(MSD).

Kwa mujibu wa Hospitali ya Wilaya ya Manyoni ni kwamba MSD wamepeleka vifaa vya kisasa ambavyo vimewezesha kurahisisha huduma kwa wateja(wagonjwa) ikiwemo mashine yenye uwezo wa kupima sampuli nane kwa wakati mmoja hali ambayo pia imesaidia kupunguza msongamano.

Akizungumza katika ziara ya kikazi iliyoandaliwa na MSD ya kutembelea hospitali hiyo, Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni mkoani Singida Dk.Bwire Robert amesema MSD wamefanya mageuzi makubwa ya kiutendaji katika usambazaji wa dawa na vifaa tiba katika hospitali, vituo vya afya na Zahanati nchini. 

Amesisitiza mabadiliko yaliofanywa na MSD yamewarahisishia wao kama watoa huduma za afya kwa wananchi kufanyakazi zao kwa kujiamini huku malalamiko ya wananchi kuhusu huduma yakipungua kwa kiasi kikubwa.

Dk.Bwire kwa sasa MSD wanafanyakazi kidijitali jambo ambalo linarahisisha mpaka ngazi ya kijiji kutoa oda ya dawa na kufanyiwa kazi ndani ya muda mfupi na hatimaye kupata dawa na vifaa tiba. 

“Kumekuwa na mapinduzi makubwa katika utoaji huduma kutokana na Serikali kuwekeza katika vifaa tiba,  dawa na watoa huduma.”

Akieleza zaidi Dk.Bwire amesema uamuzi wa MSD kuwezesha uwepo wa chumba maalum na vifaa tiba kwa ajili ya kuhudumia watoto njiti umewezesha sasa watoto hao kuhudumiwa vema na kukua bila changamoto yeyote na kusisitiza hivi sasa hata mtoto mwenye gramu 600 wana uhakika atahudumiwa,atakuwa salama.

“MSD imetuletea vifaa maalum vya kuwatunzia watoto njiti na uwepo wa vifaa hivyo tumepunguza vifo vya watoto njiti kwa asilimia 90,haya ni mafanikio makubwa sana katika sekta ya afya.Tunaipongeza Serikali yetu inayoongozwa na Rais Samia kwani kupitia MSD huduma za afya zimekuwa bora na za uhakika.”

Pamoja na hayo amesema pia MSD imewezesha hospitali ya Wilaya ya Hospitali Manyoni kuwa na vifaa vya maabara vya kisasa ikiwemo mashine za UtraSound ya kisasa, mashine za upasuaji, na Mashine ya usingizi . 

Kuhusu vitanda vyenye mashine za kupumulia amesema wanavyo vya kutosha hivyo kwao sio changamoto tena huku akieleza kuwa uamuzi wa MSD kujenga chumba cha kisasa cha kuhifadhia maiti imesaidia miili ya wapendwa wetu kuhifadhiwa sehemu salama katika hospitali hiyo.

Awali Meneja MSD kanda ya Dodoma Mwanashehe Jumaa amefafanua kwamba MSD inahudumia  vituo zaidi ya 400 kwa Mkoa wa Singida huku Kanda Nzima ya Kati ikiwemo Mkoa wa Singida, Dodoma na Wilaya ya Kiteto ikiwa na jumla ya vituo zaidi ya 840.

Kwa wa upande wa wananchi wa Wilaya ya Manyoni wameipongeza Serikali kupitia MSD kwa kuendelea kuboresha huduma za afya kwa kuiwezesha Hospitali ya Wilaya kuwa na vifaa tiba vya kisasa sambamba na uhakika wa dawa kwani yale malalamiko ya kukosa huduma hayapo tena.

Wananchi hao walipoulizwa kuhudumiwa katika hospitali za serikali au binafsi wanachagua kwenda wapi wamejibu kwa sasa kimbilio lao ni katika hospitali za serikali kwani hakuna huduma ambayo wanaihitaji wameikosa kwa kuwa kuna kila kitu.






-Asema Rais Dkt. Samia ni kiongozi mbunifu na wa vitendo


WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba leo Aprili 26, 2026 anazungumza na wananchi wa mkoa wa Dar es Salaam ambapo amefanya ziara ya kikazi ya siku moja.

Akizungumza katika mkutano wa hadhara unaofanyika katika uwanja wa Shule ya Msingi Msimbazi, Dkt. Mwigulu amesema kuwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ni kiongozi wa vitendo na mwenye dhamira ya dhati ya kuwatumikia watanzania kwa kutoa majawabu ya changamoto zinazowakabili.

Aidha, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu amesema kuwa ofisi zote za umma zipo kwa ajili ya kuwatumikia Watanzania kwa kutoa majawabu ya kero za wananchi.

Awali Mheshimiwa, Dkt. Mwigulu alikagua maendeleo ya ujenzi wa Daraja la Mkwajuni lenye urefu wa mita 20 na kimo cha mita 5.5 ambalo hadi kukamilika kwake litagharimu shilingi bilioni 11.6.

Pia, Mheshimiwa Waziri Mkuu alikagua mradi wa ujenzi wa Daraja la Kigogo lenye urefu wa mita 50 kimo cha mita 8.9 na barabara unganishi zenye jumla ya urefu wa mita 625 ambalo hadi kukamilika kwake litagharimu shilingi bilioni 17.7.














Vyama 12 Vimepongeza ripoti ya tume ya kuchunguza matukio ya tarehe 29 na baada ya uchaguzi iliyowasilishwa na Jaji Chande.

Katika mkutano huo Mhe Doyo alipongeza hotuba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Samia Suluhu Hassan kwa kukubaliana na mapendekezo yote yaliyopendekezwa na tume hiyo, aidha Mhe.Doyo amesisitiza pendekezo namba nne na pendekezo namba tano mamlaka husika wayafanyie kazi haraka kuondoa mzozo uliopo wa kisiasa hapa nchini.









Na Pamela Mollel,Arusha .

Katika kuendeleza misingi ya uongozi na ushirikiano wa kikanda, Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) imefanya makabidhiano ya nafasi ya Katibu Mkuu, ambapo Veronica Nduva amekabidhi madaraka kwa mrithi wake Stephen Patrick Mbundi katika hafla iliyofanyika kwenye makao makuu ya jumuiya hiyo jijini Arusha.

Makabidhiano hayo yamehitimisha rasmi kipindi cha uongozi wa Nduva, aliyeliongoza taasisi hiyo kwa msisitizo wa kuimarisha mshikamano wa nchi wanachama na kusukuma mbele ajenda za maendeleo ya kikanda, hususan katika nyanja za uchumi na ushirikiano wa kimkakati.

Katika kipindi chake cha uongozi, hatua mbalimbali zimechukuliwa katika kuimarisha utekelezaji wa miradi ya pamoja, kukuza biashara ndani ya ukanda na kuweka mazingira rafiki ya ushirikiano wa kiuchumi kati ya nchi wanachama wa jumuiya hiyo.

Aidha, ameweka msisitizo mkubwa katika umuhimu wa kuendelezwa kwa mshikamano miongoni mwa nchi wanachama, akieleza kuwa mafanikio yaliyofikiwa yanahitaji kulindwa na kuendelezwa kupitia ushirikiano wa karibu wa wadau wote wa maendeleo ndani ya EAC.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu mpya Balozi Mbundi ameanza majukumu yake kwa kueleza dhamira ya kuharakisha utekelezaji wa ajenda kuu za jumuiya, akitaja vipaumbele vya kuimarisha soko la pamoja, kukuza biashara ya ndani ya ukanda na kuongeza ufanisi wa taasisi zake.

Ameeleza kuwa atahakikisha kunakuwepo usimamizi thabiti wa rasilimali, uwajibikaji na uwazi katika utekelezaji wa majukumu ya jumuiya, huku akihimiza ushirikiano wa karibu kati ya nchi wanachama katika kukabiliana na changamoto zilizopo.

Mabadiliko hayo ya uongozi yanakuja katika kipindi ambacho EAC inaendelea kupanuka na kuimarisha nafasi yake kikanda na kimataifa, hali inayoweka matarajio makubwa kwa uongozi mpya katika kusukuma mbele ajenda ya ujumuishaji wa kikanda na ustawi wa wananchi wake.







Na Mwandishi Wetu


Kampuni ya Taifa Gesi imeendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu matumizi sahihi na salama ya gesi, sambamba na kuhamasisha usalama mahali pa kazi katika maadhimisho ya Wiki ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi Duniani.

Akizungumza katika viwanja vya Shule ya Msingi Mji Mwema, Njombe, Mtaalamu wa Masuala ya Afya, Mazingira, Usalama na Ulinzi Mahali pa Kazi kutoka Taifa Gesi, Aurelius Marcus Mdemu, alisema kampuni hiyo imeshiriki maadhimisho hayo yanayoanza Aprili 24 hadi 29, 2026 kwa lengo la kutoa elimu kwa wateja na jamii kwa ujumla.

Alisema kupitia banda lao, wanaonesha vifaa mbalimbali vinavyotumika kazini ili kuimarisha usalama wa wafanyakazi, pamoja na kutoa elimu kuhusu matumizi sahihi ya gesi na faida zake. Aidha, alieleza kuwa wanajitahidi kuondoa hofu na dhana potofu zilizopo miongoni mwa watumiaji wa gesi.

“Tunawaonesha wananchi namna Taifa Gesi inavyoweka kipaumbele kwenye usalama wa wafanyakazi, ikiwa ni pamoja na matumizi ya vifaa kinga vinavyotakiwa kutumika muda wote wakiwa kazini,” alisema Mdemu.

Kwa upande wake, Afisa Masoko wa Chapa wa Taifa Gesi, Santina Ngaponda, alisema maonyesho hayo yameandaliwa na OSHA, yalianza Aprili 24 na yanatarajiwa kufikia kilele chake Aprili 29 mwaka huu.

Ngaponda aliwahimiza wakazi wa Njombe na maeneo ya jirani kutembelea banda la Taifa Gesi ili kupata elimu kutoka kwa wataalamu wa usalama, kujifunza matumizi sahihi ya gesi, pamoja na kuona vifaa vya usalama vinavyotumika kazini na umuhimu wake.

Aidha, aliongeza kuwa kampuni hiyo inatoa punguzo maalum la bei ya gesi na vifaa vyake, pamoja na zawadi mbalimbali kwa wateja watakaotembelea banda hilo.

Naye Meneja Mauzo wa Kanda ya Nyasa wa Taifa Gesi, Arnold Salewa, alisema wanaendelea kutumia maonyesho hayo kutoa elimu kuhusu matumizi sahihi ya nishati safi pamoja na kuuza bidhaa zao kwa bei ya promosheni.

Alisema kanda hiyo inajumuisha mikoa ya Njombe, Iringa na Ruvuma, na kwamba pia wanatoa fursa kwa wananchi wanaotaka kuwa mawakala wao, kwa kuwapatia elimu ya biashara na usimamizi salama wa mitungi ya gesi.

Salewa alisisitiza kuwa Taifa Gesi ipo mstari wa mbele kuhakikisha kaya, migahawa na taasisi mbalimbali zinaanza kutumia nishati safi ya kupikia kwa gharama nafuu, ili kupunguza athari za matumizi ya mkaa na kuni kwa mazingira na afya za Watanzania.

Aliongeza kuwa mwitikio wa wananchi umekuwa mkubwa, huku Taifa Gesi ikiendelea kuwa chaguo sahihi kwa watumiaji wengi nchini.

Top News