Serikali ya Mkoa wa Dodoma imewataka wafanyabiashara, wawekezaji, washauri wa kodi na wananchi kuendelea kushirikiana na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kwa kuzingatia sheria za kodi ili kuongeza mapato ya Serikali na kuchochea maendeleo ya Taifa.
Wito huo umetolewa na Mkuu wa Wilaya ya Chamwino, Mhe. Janeth Mayanja, aliyemwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Dodoma katika maadhimisho ya miaka 30 ya TRA na hafla ya utoaji wa Tuzo za Mheshimiwa Rais kwa Walipakodi Bora,Julai 1, 2026 Jijini Dodoma.
Mhe. Mayanja amesema wafanyabiashara wanapaswa kusajili biashara zao kwa mujibu wa sheria, kutunza kumbukumbu sahihi za biashara, kuwasilisha ritani za kodi kwa wakati na kulipa kodi kwa hiari, kwa wakati na kwa usahihi.
Aidha, amewahimiza kutumia mifumo rasmi ya Serikali katika kufanya malipo, kutumia mashine za EFD ipasavyo na kutoa risiti halali kwa kila mauzo, huku akiwataka wananchi kudai risiti kila wanaponunua bidhaa au huduma na kuepuka vitendo vya ukwepaji wa kodi vinavyokwamisha maendeleo ya Taifa.
Amesema ushirikiano huo utawezesha Serikali kuongeza mapato na kutekeleza miradi mingi zaidi ya maendeleo kwa manufaa ya wananchi, huku Mkoa wa Dodoma ukiendelea kushirikiana kwa karibu na TRA kuhakikisha mazingira ya biashara yanakuwa rafiki na changamoto za walipakodi zinapatiwa ufumbuzi kwa wakati.
Kwa upande wake, Kaimu Meneja wa TRA Mkoa wa Dodoma, John Njau, amesema maadhimisho ya miaka 30 ya TRA ni fursa ya kutafakari mafanikio yaliyopatikana tangu kuanzishwa kwa mamlaka hiyo mwaka 1996, ikiwemo maboresho ya mifumo ya ukusanyaji wa mapato, matumizi ya teknolojia za kidijitali na utoaji wa huduma bora kwa walipakodi.
Njau amesema mafanikio hayo yamechangiwa na ushirikiano wa walipakodi na wadau mbalimbali, huku akiwapongeza walipakodi wanaotekeleza wajibu wao kwa hiari na waliotunukiwa Tuzo za Rais kwa Walipakodi Bora kwa kuwa mfano wa kuigwa katika kujenga uchumi wa Taifa.
Naye Mwenyekiti wa Washauri wa Kodi Mkoa wa Dodoma, CPA Dkt. Lucas Webie, amewataka wafanyabiashara kuacha kuiangalia TRA kama adui, akisema mamlaka hiyo hutoa nafasi ya kusikiliza changamoto za walipakodi na kuweka utaratibu wa ulipaji wa kodi kwa awamu, huku akisisitiza kuwa mapato ya kodi ndiyo msingi wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo nchini.




.jpeg)
.jpeg)











.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)






























.jpeg)
