Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) imeandaa futari maalum kwa watoto wenye uhitaji kutoka Kituo cha Kulea Watoto wenye Uhitaji cha Zili, tukio lililolenga kuimarisha mshikamano wa kijamii na kuendeleza ujumuishi kwa makundi yenye mahitaji maalum.

Hafla hiyo ilifanyika katika Makao Makuu ya TCAA jijini Dar es Salaam, na kuhudhuriwa na wadau wa sekta ya usafiri wa anga, watumishi wa TCAA pamoja na watoto wenye uhitaji. Wageni walishiriki futari kwa pamoja na watoto hao, pamoja na kukabidhi zawadi kama ishara ya upendo, mshikamano na uwajibikaji wa kijamii.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mgeni Rasmi Naibu Waziri wa Uchukuzi Mhe. David Kihenzile, aliyemwakilisha Waziri wa Uchukuzi, alipongeza jitihada za TCAA katika kuchangia maendeleo ya jamii akisisitiza umuhimu wa taasisi za umma kushiriki kikamilifu katika shughuli za kijamii, hususan zinazolenga kuwajali watoto wenye uhitaji.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa TCAA, Salim Msangi alisisitiza kuwa pamoja na jukumu la kusimamia na kudhibiti sekta ya usafiri wa anga, mamlaka itaendelea kutekeleza miradi ya kijamii inayolenga kugusa maisha ya wananchi na kukuza maadili ya utu, mshikamano na usawa.

Kupitia futari hii maalum, TCAA imeendelea kudhihirisha kuwa sekta ya usafiri wa anga siyo tu kuhusu usimamizi na kanuni, bali pia ni chombo muhimu cha kujenga jamii jumuishi, yenye huruma na mshikamano.
Naibu Waziri wa Uchukuzi David Kihenzile pamoja na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) Salim Msangi wakikabidhi mkono wa mwezi mtukufu kwa  watoto wenye uhitaji kutoka Kituo cha Kulea Watoto wenye Uhitaji cha Zili ikiwa ni kuimarisha mshikamano wa kijamii na kuendeleza ujumuishi kwa makundi yenye mahitaji maalum.
Naibu Waziri wa Uchukuzi David Kihenzile  akitoa neno wakati wa futari iliyoandaliwa na Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA)
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) Salim Msangi akizungumza na baadhi ya wafanyakazi wa TCAA, wadau mbalimbali wa Usafiri wa Anga pamoja na watoto wenye uhitaji kutoka Kituo cha Kulea Watoto wenye Uhitaji cha Zili wakati wa hafla ya futari iliyoandaliwa na TCAA.
Baadhi ya wafanyakazi wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), wadau mbalimbali wa Usafiri wa Anga pamoja na watoto wenye uhitaji kutoka Kituo cha Kulea Watoto wenye Uhitaji cha Zili wakiwa kwenye hafla ya futari iliyoandaliwa na TCAA.
Mjumbe wa Bodi ya TCAA Vuai A. Hilal akitoa neno la shukrani  kwenye hafla ya futari iliyoandaliwa na TCAA.
Picha za pamoja
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akijumuika na Wananchi wa Chakechake, Mkoa wa Kusini Pemba kwenye Futari aliyowaandalia pamoja na Viongozi mbalimbali, tarehe 13 Machi, 2026.











Viongozi mbalimbali pamoja na wananchi wa Chakechake, wakiwa kwenye Futari iliyoandaliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika Kiwanja cha Kufurahisha watoto Tibirinzi, Mkoa wa Kusini Pemba, tarehe 13 Machi, 2026.

Waziri wa Afya, Mhe. Mohamed Mchengerwa, amesema mfumo wa “Ongea na Waziri” ni daraja muhimu kati ya serikali na wananchi unaolenga kusikiliza moja kwa moja maoni, kero na mapendekezo ya wananchi kuhusu huduma za afya.

Amesema mfumo huo, uliozinduliwa rasmi Januari 26, 2026, unalenga kuongeza uwazi na uwajibikaji katika utoaji wa huduma za afya na kuhakikisha maamuzi ya serikali yanaendana na mahitaji halisi ya wananchi.


Waziri Mchengerwa ametoa kauli hiyo Machi 13, 2026 wakati wa ziara yake katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Mwananyamala jijini Dar es Salaam, ambapo pia alishiriki katika tukio la “Ongea na Waziri” lililowakutanisha watumishi wa afya na wananchi kwa lengo la kusikiliza changamoto na kupokea maoni kuhusu utoaji wa huduma za afya.

Amesema kuanzishwa kwa mfumo huo kunaonesha dhamira ya serikali ya kuweka kipaumbele katika kusikiliza wananchi kama msingi wa kuboresha huduma na kuimarisha uwajibikaji katika sekta ya afya.

Aidha, Waziri Mchengerwa amesema serikali ipo mbioni kuandaa mwongozo utakaotumika katika hospitali zote za serikali ili kukabiliana na malalamiko ya wananchi kuhusu gharama kubwa za matibabu na upatikanaji wa dawa. 



Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Dkt. Seif Shekalaghe, amesema mfumo wa kidijitali wa “Ongea na Waziri” ulioanzishwa na Waziri Mchengerwa unalenga kusikiliza na kutatua changamoto zinazowakabili wananchi katika sekta ya afya.

Dkt. Shekalaghe amesema kupitia mfumo huo wananchi wanapata nafasi ya kuwasilisha changamoto na maoni yao moja kwa moja kwa Waziri, jambo linalosaidia kupatikana kwa ufumbuzi wa haraka na kuimarisha utoaji wa huduma za afya.

Ameongeza kuwa wizara itafanya majumuisho ya maswali yaliyoulizwa katika mwezi uliopita ili kutathmini ni maswali mangapi yamepatiwa majibu pamoja na hatua zilizochukuliwa katika kuyatatua.

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Hospitali ya Mwananyamala, Evancy Asenga, amemshukuru Waziri Mchengerwa kwa ziara yake hospitalini hapo na kuahidi kutekeleza maagizo yote yaliyotolewa ili kuboresha huduma, hususan katika eneo la mapokezi ya wananchi.

Pia ameomba serikali kufanikisha ujenzi wa jengo kubwa la ghorofa katika hospitali hiyo ili kurahisisha utoaji wa huduma. 



Asenga amesema hospitali hiyo imefanikiwa kufanya mageuzi makubwa katika utoaji wa huduma kutokana na uwekezaji mkubwa uliofanywa na serikali ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Kwa upande wake, Kaimu Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Mwananyamala, Dkt. Mercy Maya, amesema hospitali hiyo inaendelea kuimarisha na kupanua huduma za kibingwa kwa kuboresha miundombinu na kuongeza vifaa tiba ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora kwa wakati.


Mwandishi Wetu,
Dar es Salaam. 
TAKWIMU kutoka cha Kituo cha Udhibiti wa Magonjwa Afrika (CDC-Afrika) zinaonyesha kuwa, vifo vya uzazi Tanzania vimepungua kwa asilimia 80 kutoka 556 katika kila vizazi hai 100000 mwaka 2016 hadi 104 katika kila vizaizi hai 100000 mwaka 2022.

Katika mgawanyo wa vifo 556 katika kila vizazi hai 100,000, kwa mwaka ni sawa na vifo 2 kila siku vinavyotokana na uzazi kwa kinamama.

Laiti ingekuwa basi la moja la abiria kila linapokwenda katika safari zake linapata ajali na kuua watu wawili kila siku, basi hilo lingetazamwa kama janga kubwa kwa taifa na maswali mengi angehojiwa dereva na mmiliki wa basi.

Na hali hiyo ndiyo iliyosababisha serikali kuamua kulivalia njuga suala la vifo vya uzazi kwa kinamama.

Kwa mujibu wa Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mwananyamala, Irene Barongo, vifo vya uzazi kwa kinamama vilikuwa saba katika mwaka wa fedha, 2023/2024 na mwaka jana, kulikuwa na vifo vitatu tu.

“Kuna mengi yamefanywa, kwa kupitia ‘Mama Samia Sponsorship’ madaktari bingwa wamesomeshwa ambao wanarudi katika hospitali, hali ambayo imechangia kupunguza vifo vya uzazi kwa kiasi kikubwa,” amesema.

Kwa upande wa watoto kadhalika, Hospitali ya Mwananyamala imepunguza vifo vya Watoto. Daktari Bingwa wa Watoto Makena Kato anasema, awali walikuwa wakitegemea vifaa vya kupumulia kwa watoto wenye changamoto kupumua(sipap).

Dk Kanto anasema, awali walikuwa wakitegemea ‘sipap’ moja tu na sasa serikali imeongeza machine zaidi ya 20.

“Kwa mfano mtoto amezaliwa na changamoto ya upumuaji labda kwa sababu alizaliwa kabla ya wakati au njiti, halafu hospitali ina sipap moja, basi hapo ni kupanga foleni, kusubiri mtoto aliyewekwa atoke. Kwa hali ile ni rahisi Watoto kufariki.” anasema

Lakini Dk Kanto anaongelea umuhimu wa afya na uhai wa mama wakati wa kujifungua na kusema, Mungu amemuumba mwanamke kwa namna ya kipekee ili alete uhai duniani, hivyo kupoteza maisha wakati wa kitendo hicho si haki.

Mganga Mfawidhi Mwananyamala, Dk Barongo anafafanua zaidi jinsi ambavyo Mwananyamala wameingilia kati vifo vya uzazi kwa kinamama na kusema kampeni kubwa imefanyika katika suala la kukusanya damu salama,jambo ambalo limepunguza vifo vya uzazi.

Anasema kwa mwaka hospitali inazalisha wanawake kuanzia 5000 mpaka 6000, na vifo vinavyotokea kwa kiasi kikubwa havisababishwi na ukosefu wa damu.

Akiuzungumzia mwezi wa maadhimisho ya wanawake duniani, Dk Barongo anasema, hakuna jambo gumu kama pale ambapo mjamzito anajifungua na kisha anafariki dunia na kumuacha mtoto.

“Lazima ndani ya saa 24, lazima tukae, tuitane, tuulizane nini kimetokea, tunaiita ‘mortality review’ tunaangalia tumekosea wapi. Cha muhimu kusiwepo na vifo vya wanawake wakati wa uzazi, kwa sababu mama kama kiumbe anayeleta uhai duniani, hastahili kufa”anasema na kuongeza:

“Kikitokea kifo cha mwanamke wakati wa kujifungua na akabaki mtoto salama, tunajiuliza maswali mengi, huyu mtoto atabaki na nani, atanyonya nini? Atalelewa na nani? Ni vifo vinavyoumiza sana”

Dk Barongo anasema katika kupunguza vifo vya uzazi hata wauguzi na madaktari wanasimamiwa katika kubadili mitazamo na kuondoa lugha chafu kwa wagonjwa wakiwamo wajawazito.

Anaongeza kuwa, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan alilibeba suala la afya ya uzazi kwa kinamama kama mama akitambua nafasi ya uzazi kwenye jamii.

“Kwa kweli katika awamu hii tumeona, yule ni mama na ninavyoona katika uongozi wake ameamua kumuangalia mama na mtoto, na kiuhalisia katika uwekezaji uliowekwa kwenye sekta ya afya, hakuna kifaa ambacho tutakiomba tukanyimwa na hiyo imesaidia sana kupunguza vifo vya kinamama,” anasema na kuongeza:

‘Kila mahali mama Samia amewekeza kwenye afya ya mama na mtoto, kwa kweli kama ni kutajwa kuwa kinara wa afya ya mama na mtoto anastahili,”

Malengo ya Maendeleo Endelevu(SDG) inataka nchi za Afrika kupunguza vifo vya uzazi hadi kufikia 70 katika kila vizazi hai 100,000. Lakini Tanzania bado haijafikia lengo hilo ingawa jitihada za dhati na matokeo yameonekana kwa asilimia 80.

HOSPITALI YA AMANA
Mkunga Mbobezi, Joyce Njenga wa Hospitali ya Rufaa ya Amana anasema, miaka mitano iliyopita, Amana ilikuwa ina idadi kubwa ya vifo vya uzazi kwa kinamama, kwa mfano mwaka 2023, kinamama 12 walifariki kwa mwaka kwa sababu ya uzazi na mpaka mwaka jana kulikuwa na vifo viwili tu.

“Hii inatokana na kuongezwa kwa vifaa tiba ikiwamo machine ya ‘ultrasound’ kingine ni ushirikiano katika kufanya kazi, akifika tu anaangaliwa anahitaji huduma gani, kwa wanaohitaji upasuaji, ndani ya nusu saa anaandaliwa na kupelekwa chumba cha upasuaji” anasema

Anasema katika hospitali ya Amana kuna madaktari bingwa wa nane wa masuala ya uzazi na wakunga wabobezi watatu.

“Zamani mkunga mmoja anazalisha Watoto sita hadi saba peke yake, sasa hivi huduma za afya zimeimarishwa zaidi katika hospitali za pembezoni na kusaidia kupunguza mzigo wa wagonjwa katika hospitali za rufaa” anasema.
Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Amana, Dk Bryson Kiwale anasema vifo 556 ni sawa na mabasi kadhaa ya abiria yaanguke na yasababishe vifo.

Anasema, kama mabasi hayo yangeanguka na kuua, pengine ungetangazwa msiba mzito kwa taifa lakini kwa sababu ni msiba unaoikuta familia moja, na sehemu nyingine familia moja, watu hawaoni ukubwa wa vifo hivi.

“Ni dhamira ya kweli ya serikali na wala hakuna muujiza, serikali imeamua kuwekeza katika afya ya msingi, ikiwamo mafunzo na utayari wa watoa huduma katika sekta ya afya,” anasema

Daktari Bingwa wa Watoto, Hospitali ya Amana, Grace Mhando anasema ingawa vifo vya watoto bado ni changamoto lakini vimepungua.

Anasema kwa sasa Tanzania inazungumzia vifo vya Watoto 24 katika kila vizazi hai 1000 hali ambayo bado tunaweza kusema bado hatujafikia lengo la kidunia la kupunguza vifo hivyo hadi kufikia 12 katika kila vizazi hai 1000.

“Lakini tumeona juhudi za serikali, kwa kupitia ‘Mama Samia Sponsorship’ madaktari bingwa wanaendea mpaka vijijini kuwahudumia Watoto ambao wana hali ya chini.

Ripoti iliyochapishwa Januari mwaka 2025 na Jarida la Afya la Uingereza, imeonyesha kuwa program zilizofanyika zikihusisha serikali, taasisi za afya na wataalamu wa afya, zimewezesha kupunguza kwa asilimia 75 vifo vya uzazi katika kipindi cha miaka mitatu.

Utafiti huo ulifanywa katika vituo 30 vya afya vinavyopokea wagonjwa wengi Tanzania na matokeo yalibainisha kuwa maelfu ya kinamama waliepuka vifo vya uzazi kwa kutumia program zilizowekwa na vifaa tiba vilivyotolewa na serikali na wadau wa maendeleo.

Februari mwaka jana, Taasisi ya Gates, ilimpa Rais Samia Suluhu tuzo maalum ya Goalkeepers ya kutambua mchango wake katika kuboresha afya ya mama na mtoto na lishe. Rais aliitoa tuzo hiyo kwa wafanyakazi wote wa sekta ya afya kwa mchango wao katika kupunguza vifo hivyo.

📍Yasifu uwekezaji wa shilingi bilioni 429


NA MASHAKA MHANDO, Tanga

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu imeiashauri Serikali kuongeza kasi ya utatuzi wa changamoto za miundombinu wezeshi katika Bandari ya Tanga, ili kuendana na kasi ya ongezeko la shehena na meli kubwa zinazoingia bandarini hapo kufuatia maboresho makubwa yaliyofanyika.

Ushauri huo umetolewa Leo Machi 13 na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Profesa Joyce Ndalichako, wakati wa ziara ya kikazi ya kukagua utendaji na ufanisi wa bandari hiyo, ambayo hivi sasa imekuwa mbadala muhimu katika kupunguza msongamano wa mizigo kwenye Bandari ya Dar es Salaam.

Akizungumza baada ya kukagua gati jipya, Profesa Ndalichako alipongeza uwekezaji wa Shilingi Bilioni 429 uliowekwa na Serikali ya Awamu ya Sita, akisisitiza kuwa ni lazima kasi ya ujenzi wa barabara za kuingia na kutoka bandarini iongezwe ili kurahisisha usafirishaji wa mizigo kwenda kwa walaji.

“Kamati inampongeza Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa maono yake ya kuifungua Tanga. Tunaunga mkono mpango wa kuunganisha bandari hii na reli ya kisasa ya SGR kutoka Tanga hadi Musoma, hatua itakayochochea tija na ajira kwa wingi,” alisema Profesa Ndalichako.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Uchukuzi,  David Kihenzile, alibainisha kuwa Serikali inaendelea na mpango wa kuunganisha bandari hiyo na mtandao wa reli wa kilomita 248 (Tanga–Mruazi–Ruvu) na hatimaye kufika Arusha. Alieleza kuwa reli ya SGR kupitia Minjingu na Engaruka hadi Musoma itakuwa kiunganishi muhimu cha kiuchumi.

Meneja wa Bandari ya Tanga,  Salehe Mbega, alieleza kuwa maboresho hayo yameongeza kina cha maji kufikia mita 12, hali inayoruhusu meli kubwa zenye urefu wa hadi mita 200 kutia nanga, tofauti na hapo awali.

“Ufanisi umeongezeka kiasi kwamba meli sasa zinahudumiwa ndani ya siku tatu hadi tano. Hata hivyo, kutokana na ubora wa huduma zetu, mahitaji yameongezeka na wakati mwingine hadi meli 14 husubiri nje ya bandari. Ili kutatua hili, tuna mpango wa kujenga magati matatu mapya na kituo cha kisasa cha abiria (Terminal) katika awamu ya tatu ya mradi,” alisema Mbega.

Maboresho hayo yanatajwa kuwa kichocheo kikubwa cha uchumi wa mkoa wa Tanga, yakigusa sekta za usafirishaji, biashara ndogondogo, na kuimarisha nafasi ya mkoa huo kama kitovu cha uwekezaji nchini. 







Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rose Senyamule, ametoa wito kwa wazazi na walezi kuwa makini na watoto wao wakati wa msimu wa mvua ili kuepuka ajali zinazoweza kusababisha vifo, kufuatia watoto wawili wadogo kufariki dunia baada ya kuzama kwenye madimbwi ya maji.

Akizungumza wakati wa ziara yake ya kukagua maeneo yaliyoathiriwa na mvua Kata ya Nzuguni Halimashauri ya Jiji la Dodoma, leo Machi 13, 2026, amesema ni muhimu kwa wazazi kuhakikisha watoto hawachezi kwenye madimbwi au maeneo yenye maji mengi kipindi hiki cha mvua ili kuwalinda dhidi ya hatari zinazoweza kutokea.

Aidha, amewataka wananchi kutunza mazingira na kuepuka kuchafua mifereji ya maji kwa kutupa taka ovyo, akieleza kuwa hali hiyo huchangia kuziba mifereji na kusababisha maji kujaa katika makazi ya watu pamoja na barabarani.

Amesema pamoja na changamoto zinazosababishwa na mvua, bado wananchi wanapaswa kuona kuwa mvua ni neema kwa Jiji la Dodoma kwa kuwa inaongeza uzalishaji wa chakula na kuleta ukijani kwenye mazingira.

Katika hatua nyingine, amewataka baadhi ya wananchi waliovamia na kujenga kwenye njia za maji kuzingatia sheria za mipango miji ili kuepusha madhara yanayotokea wakati wa mvua, ikiwemo nyumba kujaa maji.

Ametoa pole kwa wananchi waliokumbwa na athari za mvua na kuwataka kuwa na uvumilivu wakati Serikali ikiendelea na jitihada za kutatua changamoto hizo. Amesema suluhisho la kudumu litatekelezwa mara mvua zitakapopungua kunyesha ili kuruhusu utekelezaji wa maboresho ya miundombinu ya barabara na mifereji ya maji.

Akisoma taarifa kwa Mkuu wa Mkoa, Mtendaji wa Kata ya Nzuguni, Edgar Fungo, amesema kuanzia Januari 21, 2026 hadi Machi 13, 2026, jumla ya kaya 271 zimeathirika na maafa ya mvua katika kata hiyo. Kati ya hizo, nyumba 42 zimeezuliwa na upepo, nyumba 170 zimeingiliwa na maji na nyumba 59 zimebomoka.

Ameeleza kuwa mvua kubwa iliyonyesha Februari 9, 2026 iliathiri maeneo ya Mtaa wa Kitelela, Nzuguni C na Mahomanyika ambapo katika eneo la Kitelela barabara ziliharibika na kusababisha kushindwa kupitika, hali iliyosababisha wanafunzi kushindwa kwenda shule baada ya korongo kujaa maji pamoja na wananchi kukosa huduma za msingi.

Kwa upande wa Mahomanyika, daraja lilivunjika na kusababisha shughuli mbalimbali kusimama, huku katika eneo la Nzuguni C mfereji wa maji uliochimbwa kuzunguka ukuta wa Nane Nane ulijaa na kusababisha maji kusambaa hadi kwenye makazi ya wananchi.

Aidha, amesema Mbunge wa Jimbo la Mtumba, Anthony Mavunde, kwa kushirikiana na uongozi wa kata pamoja na diwani wa kata hiyo walitembelea maeneo yaliyoathirika na kutoa pole kwa wananchi pamoja na kusikiliza changamoto zao.

Amesema ushirikiano kati ya Serikali, viongozi wa eneo pamoja na taasisi mbalimbali ni muhimu katika kuhakikisha wananchi wanaopata madhara wanapatiwa msaada na hatua za kudumu zinachukuliwa ili kupunguza athari za mafuriko katika maeneo hayo siku zijazo.




‎Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida, Dkt. Fatuma Mganga amewataka watumishi wa Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) mkoani Singida kutambua kuwa sekta ya barabara ni kiungo muhimu cha maendeleo ya sekta nyingine kama elimu, afya na uchumi, hivyo wanapaswa kutekeleza majukumu yao kwa bidii na weledi ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora.

‎Ameyazungumza hayo leo 13 Machi 2026, katika kikao kazi cha TARURA kilichofanyika katika ukumbi wa Ofisi ya Ukaguzi mkoa wa Singida ambapo Dkt. Mganga amesema TARURA ni taasisi mtambuka na inategemewa na sekta nyingi, hivyo utekelezaji mzuri wa majukumu yao ni muhimu kwa maendeleo ya jamii.

‎Amesema moja ya changamoto kubwa inayowakabili wananchi ni uwepo wa barabara zisizopitika, hivyo watumishi wa TARURA wanapaswa kuhakikisha wanakuwa karibu na maeneo ya kazi hasa katika kipindi cha mvua ili kufuatilia hali ya barabara na kuhakikisha zinaendelea kupitika.

‎‎Pia, amesisitiza umuhimu wa watumishi wa umma kuzingatia maadili ya utumishi wa umma, kuwa na mawasiliano mazuri na kuwahudumia wananchi kwa heshima akisisitiza kuwa “mteja ni mfalme”. 

Aidha, amewakumbusha watumishi kupambana na vitendo vya rushwa, kuheshimu muda wa kazi na kujaza taarifa katika mfumo wa PEPMIS ili kufikia malengo ya utendaji kazi.

‎Dkt. Mganga pia amesisitiza umuhimu wa watumishi wa umma kutunza afya zao kwa kufanya mazoezi, kupima afya mara kwa mara na kuepuka matumizi ya pombe kupita kiasi, akieleza kuwa serikali inawekeza rasilimali nyingi katika kuwajenga watumishi wake hivyo wanapaswa kulinda afya zao ili kuendelea kulitumikia taifa.

‎Awali, Meneja wa TARURA Mkoa wa Singida, Mhandisi Claver Mwinuka, amesema kikao kazi hicho kinalenga kujadili mipango ya kazi, bajeti ya mwaka ujao wa fedha pamoja na mikakati mipya ya utekelezaji wa majukumu kwa kuzingatia maelekezo ya Bodi ya Barabara mkoa wa Singida.

‎Ameongeza kuwa kikao hicho pia kitatoa fursa ya kuimarisha mahusiano na mawasiliano kati ya watumishi, hususani wapya pamoja na kujadili matumizi ya teknolojia ya mawe katika ujenzi wa barabara ili kupunguza gharama na kuboresha ubora wa miundombinu.

‎Baadhi ya washiriki wa kikao hicho wakiwemo Meneja wa TARURA Wilaya ya Iramba Mhandisi Evance Kibona na Meneja wa TARURA Wilaya ya Mkalama Mhandisi Rahabu Thomas, wamesema kikao hicho kitasaidia kuboresha utendaji kazi na kuongeza ubunifu katika ujenzi wa barabara, hususani kwa kutumia rasilimali za mawe zinazopatikana kwa wingi mkoani Singida ili kuongeza ubora wa barabara na kurahisisha usafirishaji wa mazao ya kilimo.












Top News