

Na. Philipo Hassan - Mikumi
Mwisho mwa wiki ikiyopita, Kamishna wa Uhifadhi TANAPA CPA Musa Nassoro Kuji alizindua rasmi mradi wa kusafirisha na kusambaza umeme wa TANESCO ndani Hifadhi ya Taifa Mikumi. Mradi huo unaolenga kuboresha utoaji wa huduma ndani ya hifadhi, kuimarisha shughuli za uhifadhi na utalii, kuboresha matumizi ya nishati ya umeme kwa watumishi wa hifadhi na kuongeza fursa za uwekezaji katika sekta ya utalii.
Usambazaji wa umeme wa TANESCO ndani ya hifadhi utaboresha na kuleta mapinduzi makubwa kwenye upatikanaji wa nishati hiyo kwa watumishi, watalii, wawekezaji waliopo ndani ya hifadhi hiyo pamoja na wananchi ambao nao wamefaidika na umeme huo ambao pia umepita kwenye maeneo yao wakati wa utekelezaji wa mradi huo.
Uzinduzi huo ulihudhuriwa na Menenejimenti ya hifadhi, Maafisa na Askari wa uhifadhi wakiongozwa na Kamishna Msaidizi wa Uhifadhi Augustine Masesa ambaye ndiye Mkuu wa Hifadhi ya Taifa Mikumi, Meneja wa TANESCO Morogoro Kusini Mhandisi Lugata Masingija pamoja na wananchi wa maeneo jirani na hifadhi hiyo.
Kamishna Kuji aliishukuru Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuidhinisha bajeti ya mradi huo pia Bodi ya Wadhamini ya TANAPA kwa usimamizi wa karibu wa shughuli za Shirika ikiwemo utekelezaji wa mradi huo.
Aidha, Kamishna Kuii aliupongeza uongozi wa TANESCO kwa utekelezaji wa mradi huo ambapo mbali na kuunga mkono jitihada za Serikali za uwepo wa nishati safi utaongeza kasi ya maendeleo kwa wananchi wa vijiji jirani vilivyonufaika na mradi huu,” alisema Kamishna Kuji.
Mradi huo unaweka historia mpya katika Hifadhi ya Taifa Mikumi kwa kuimarisha matumizi ya nishati safi na uhakika, hatua inayotarajiwa kuongeza ubora wa huduma, kuchochea uwekezaji wa utalii na kuendelea kufungua fursa za maendeleo kwa jamii zinazozunguka hifadhi hiyo.
Serikali kupitia Bohari ya Dawa (MSD) itaendelea kununua dawa zinazozalishwa na wawekezaji wa ndani ili kuimarisha uzalishaji wa ndani wa bidhaa za afya na kupunguza utegemezi wa bidhaa kutoka nje ya nchi.
Hayo yamesemwa Waziri wa Afya, Mohammed Mchengerwa leo Mei 11 2026 akiwasilisha Hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Afya kwa mwaka wa fedha 2026/27 Bungeni, Jijini Dodoma.
“Serikali imejipanga kuhakikisha MSD inanunua kwanza dawa zinazozalishwa ndani ya nchi zilizokidhi viwango vya Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA) kabla ya kwenda kununua kutoka nje ya nchi, hatua inalenga kukuza viwanda vya ndani, kuongeza ajira na kuimarisha uchumi wa Taifa” amesema Waziri Mchengerwa
Amesema Serikali itaendelea kuweka mazingira rafiki na wezeshi kwa wawekezaji wa ndani na nje ya nchi, ikiwemo kuboresha upatikanaji wa ardhi, miundombinu muhimu pamoja na kuratibu uwekezaji katika sekta ya dawa na bidhaa za afya ili kuvutia uwekezaji zaidi nchini.
Waziri Mchengerwa amesema Serikali imeendelea kuimarisha upatikanaji wa bidhaa za afya nchini kwa kutoa Shilingi trilioni 1.4 kupitia MSD ili kuhakikisha wananchi wanapata dawa na bidhaa muhimu za afya kwa wakati.
“Upatikanaji wa bidhaa muhimu za afya umeongezeka kutoka asilimia 58 mwaka 2021/22 hadi asilimia 88 mwezi Machi 2026” amesema Waziri Mchengerwa.
Amesema kuwa Wizara ya Afya itaendelea kuhamasisha wawekezaji wa ndani na nje ya nchi pamoja na kuwawekea mazingira rafiki na wezeshi, ikiwemo upatikanaji wa ardhi na miundombinu muhimu, ili kuwavutia kuwekeza katika ujenzi wa viwanda vya bidhaa za afya na kupunguza utegemezi.
Waziri Mchengerwa amesisitiza kuwa dhamira ya Serikali ni kuhakikisha kila Mtanzania anapata huduma bora za afya, dawa salama na huduma zenye ubora bila kuachwa nyuma.
-Wajadili Kilimo himilivu na uendelezaji wa Kilimo Biashara
WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, leo Mei 11, 2026 amekutana na Rais wa Shirika la Kimataifa la Maendeleo ya Kilimo (IFAD), Alvaro Lario, jijini Nairobi, Kenya, ambapo wamejadili maeneo mbalimbali ya ushirikiano katika sekta ya kilimo na uwezeshaji wa wananchi kiuchumi.
Katika mazungumzo hayo, Dkt. Mwigulu amesema Tanzania itaendelea kushirikiana na IFAD katika maeneo mbalimbali ikiwemo kilimo himilivu cha tabianchi, maendeleo ya kilimo biashara, mapinduzi ya kidijitali katika sekta ya kilimo pamoja na uwezeshaji wa vijana na wanawake kiuchumi.
Aidha, Waziri Mkuu amesema Tanzania inatarajia kuendelea kushirikiana na IFAD katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo ya kilimo ikiwemo mpango wa kuongeza uzalishaji wa alizeti ili kusaidia kuongeza upatikanaji wa mafuta ya kula nchini.
“Kimekuwa ni kikao kizuri kwa sababu tumekuwa na ushirikiano nao kwa muda mrefu, ambapo katika kipindi kilichopita tumeshirikiana nao katika miradi mbalimbali, na hasa miradi katika sekta za uzalishaji”.
“Lakini pia tumedhamiria kuendelea kushirikiana katika kuendeleza mazao ya mchanganyiko ambayo katika miaka ya nyuma ilikuwa inachukuliwa kuwa ni mazao ya chakula peke yake, kwasasa mazao haya niya biashara na tunayafanya sehemu ya kukuza biashara ambayo Tanzania inafanya na nchi nyingine”
Ameongeza kuwa Tanzania inatarajia kuendelea kushirikiana na IFAD katika sekta ya mifugo na mazao ya baharini kwa upande wa Zanzibar.
“Sambamba na hayo, tunategemea kushirikiana nao katika utekelezaji wa kilimo endelevu ambacho kinasaidia kampeni yetu ya kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi nchi”. Amesisitiza Dkt. Mwigulu
Kwa upande wa Rais wa IFAD Alvaro Lario, amesema kuwa wataendelea kuhakikisha mipango na utekelezaji wa IFAD vinaendana na malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo ya Tanzania 2050
“Kwasasa tunasubiri kusikia vipaumbele ya Tanzania ili tujue namna gani tunaweza kusaidia katika maeneo vya utoshelevu na usalama wa chakula pamoja na uongezaji thamani wa mazao”.
Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Dodoma imewataka watu wenye changamoto ya kusikia kutumia elimu ya kodi kama nyenzo ya kuwawezesha kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi na maendeleo ya Taifa, huku ikisisitiza umuhimu wa kila mwananchi kushiriki katika kujenga Taifa kupitia ulipaji wa kodi kwa hiari kulingana na sheria na taratibu zilizowekwa.
Akifungua semina ya elimu ya kodi kwa jamii ya watu wenye changamoto ya kusikia Mei 11, 2026 jijini Dodoma, Meneja wa TRA Mkoa wa Dodoma, Bw. Pendolake Elinisafi, amesema Serikali inaendelea kuhakikisha huduma za kodi zinawafikia wananchi wote kwa usawa ili kuongeza uelewa wa masuala ya kodi na kuwajengea uwezo wa kutumia huduma mbalimbali zinazotolewa na mamlaka hiyo.
Amesema kodi ni nguzo muhimu ya maendeleo ya Taifa kwani fedha zinazokusanywa kupitia kodi husaidia kugharamia huduma za kijamii ikiwemo elimu, afya, maji, barabara pamoja na huduma nyingine muhimu zinazogusa maisha ya wananchi kila siku.
Aidha, amepongeza ushiriki wa watu wenye changamoto ya kusikia katika semina hiyo huku akiwahimiza kutumia fursa hiyo kuuliza maswali, kutoa maoni na kujifunza zaidi kuhusu umuhimu wa ulipaji kodi kwa maendeleo ya nchi.
Kwa upande wao, baadhi ya washiriki wa semina hiyo wameishukuru TRA kwa kuandaa mafunzo hayo wakisema yatawasaidia kuelewa vyema masuala ya kodi na namna ya kupata huduma mbalimbali zinazotolewa na mamlaka hiyo bila vikwazo.

Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma
Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega amesema ameridhishwa na mafanikio ya Shindano la Ubunifu lililoanzishwa na Wizara yake kwa lengo la kuwashirikisha wanafunzi wa fani za uhandisi na ujenzi katika kutoa mawazo ya maendeleo ya miundombinu nchini.
Akizungumza kuhusu dhamira ya shindano hilo, Ulega amesema lengo kuu lilikuwa ni kukutana na wanafunzi wa taaluma za uhandisi pamoja na ukadiriaji majengo ili kuwapa uelewa kuhusu miradi mikubwa inayotekelezwa na Serikali, sambamba na kusikiliza maoni na ubunifu wao kuhusu maendeleo ya sekta ya ujenzi nchini.
Ulega Amezungumza hayo jijini Dodoma wakati wa hafla ya utoaji zawadi kwa washindi wa Shindano la andiko la ubunifu wa kupunguza msongamano wa magari mijini ambapo amesema wakati wa kuanzisha mpango huo kulikuwa na baadhi ya watu waliobeza hatua hiyo wakidai Serikali haina mipango madhubuti hadi kufikia hatua ya kutafuta mawazo kutoka kwa wanafunzi, huku baadhi ya viongozi wa upinzani wakikosoa vikali mpango huo.
Hata hivyo, Ulega amesema Wizara imeamua kuwapa nafasi vijana kutokana na uwezo wao mkubwa wa kufikiri, kubuni na kutoa suluhisho la changamoto mbalimbali zinazohusu maendeleo ya Taifa.
Amesema mwitikio wa wananchi na wadau ulikuwa mkubwa, hali iliyosababisha Wizara kupokea simu nyingi za pongezi kutoka kwa watu na taasisi mbalimbali zilizovutiwa na hatua ya kuwashirikisha vijana katika masuala ya maendeleo ya miundombinu.
Aidha, amesema mafanikio ya shindano hilo yamevutia taasisi mbalimbali ikiwemo mabenki kuamua kuunga mkono mpango huo kwa kutoa zawadi mbalimbali kwa washindi na washiriki, zikiwemo fedha taslimu za mamilioni ya shilingi pamoja na kompyuta mpakato.
Ulega amesema Rais Samia Suluhu Hassan amekuwa mstari wa mbele kuhimiza ubunifu na ushiriki wa vijana katika ujenzi wa Taifa, jambo lililoipa Wizara motisha ya kuendelea kutoa nafasi kwa vijana kushiriki katika miradi ya maendeleo.
Pia amesema Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Adolf Mkenda alimpongeza kwa hatua hiyo kupitia simu na hata kumwandikia barua rasmi ya pongezi, jambo alilosema lilimpa faraja kubwa.
Kwa mujibu wa Ulega, Profesa Mkenda alieleza kuwa lengo la challenge hiyo ni kuhamasisha matumizi ya maarifa ya vijana, kuwasaidia wanafunzi kuunganisha nadharia wanazojifunza darasani na vitendo pamoja na kuchochea ubunifu katika sekta ya miundombinu.
Amesema Serikali itaendelea kuwashirikisha vijana kila inapopata nafasi kwa kuwa Tanzania ina wataalamu wengi wenye uwezo mkubwa katika sekta ya ujenzi na miundombinu.
“Wizara ya Ujenzi ni walezi wa wahandisi wote nchini. Tuna taarifa zenu zote na tutaendelea kuwalea kwa ajili ya mustakabali wa Taifa letu,” amesema Ulega.
Katika hatua nyingine, amesema Wizara ipo katika mazungumzo na wadau wa kimataifa kwa ajili ya kuandaa “master plan” ya kisasa ya madaraja na barabara yenye lengo la kujenga miundombinu ya kiwango cha kimataifa.
Ameeleza kuwa mwelekeo wa Serikali sasa ni kutoka mfumo wa barabara moja kwenda mfumo wa barabara pana zaidi zenye njia mbili kwenda na mbili kurudi ili kukidhi mahitaji ya ukuaji wa miji pamoja na uchumi.
“Kina nani wa kufanya kazi hiyo? Ni wataalamu hawa tulionao leo pamoja na ninyi mliopo madarasani,” amesema.
Aidha, amesema Serikali ya Samia Suluhu Hassan imeendelea kuwaamini vijana kwa kuwapa nafasi mbalimbali za uongozi, akibainisha kuwa karibu nusu ya mawaziri waliopo serikalini ni vijana wenye umri wa miaka 50 na chini yake.
Ulega amesema kupitia shindano hilo, vijana wengi watafunguliwa milango ya ajira na kujiajiri kupitia ubunifu na ushiriki wao katika miradi mikubwa ya maendeleo nchini.

Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma
Waziri wa Afya, Omary Mchenjgerwa amesema Serikali imeendelea kuimarisha mapambano dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza kwa kuongeza huduma za matibabu, kinga na elimu kwa jamii, hatua iliyochangia kuongezeka kwa kliniki za kisukari na shinikizo la damu nchini.
Akizungumza leo Mei 11, 2026 bungeni jijini Dodoma wakati akiwasilisha hotuba ya makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Afya kwa mwaka wa fedha 2026/2027, Mchenjgerwa amesema wizara imeendelea kuimarisha uratibu na utekelezaji wa afua za magonjwa ya kisukari, shinikizo la damu pamoja na magonjwa sugu ya mfumo wa upumuaji.
Amesema katika kipindi cha Julai 2025 hadi Machi 2026, Serikali imeanzisha kliniki mpya 130 za huduma za kisukari na shinikizo la damu, na kufanya idadi ya kliniki hizo kufikia 168 kutoka kliniki 38 zilizokuwepo katika kipindi kama hicho mwaka 2025.
Kwa mujibu wa Waziri huyo, kliniki hizo zimepatiwa dawa muhimu, vifaa tiba pamoja na mafunzo kwa watumishi wa afya ili kuboresha upatikanaji na ubora wa huduma kwa wananchi wenye magonjwa yasiyoambukiza.
Aidha, amesema Serikali imeendelea kuboresha huduma za kinga na uchunguzi wa magonjwa hayo kupitia kampeni mbalimbali za afya ikiwemo upimaji wa magonjwa yasiyoambukiza katika maeneo ya kazi, utoaji wa elimu kwa jamii pamoja na matembezi ya Kitaifa yanayohamasisha wananchi kufanya mazoezi.
Mchenjgerwa ameongeza kuwa Wizara pia imeendelea kutumia vyombo mbalimbali vya habari kutoa elimu ya uhamasishaji kwa wananchi kuhusu namna ya kujikinga na kudhibiti magonjwa yasiyoambukiza, hatua inayolenga kupunguza ongezeko la wagonjwa na madhara yatokanayo na magonjwa hayo nchini.
Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma
Serikali kupitia Wizara ya Afya imeendelea kuonyesha mafanikio makubwa katika sekta ya afya baada ya kiwango cha utoaji wa chanjo nchini kufikia asilimia 96, hatua inayotajwa kuwa ni mafanikio makubwa katika kuimarisha kinga dhidi ya magonjwa kwa watoto na wananchi kwa ujumla.
Hayo yameelezwa na Waziri wa Afya, Mhe. Mohammed Mchengerwa (MB), wakati akiwasilisha Bajeti ya Wizara ya Afya kwa mwaka wa fedha 2026/27 bungeni, ambapo amesema ongezeko hilo limetokana na juhudi za Serikali za kuimarisha huduma za msingi za afya pamoja na kuongeza upatikanaji wa chanjo katika maeneo mbalimbali nchini.
Amesema kiwango hicho kimeongezeka kutoka asilimia 93 hadi asilimia 96, jambo linaloifanya Tanzania kuvuka lengo la kimataifa la asilimia 90 lililowekwa kwa ajili ya utoaji wa chanjo.
“Kuongezeka kwa kiwango hiki ni matokeo ya uwekezaji mkubwa unaoendelea kufanywa na Serikali katika sekta ya afya, hususan kwenye huduma za kinga na chanjo ambazo zimeendelea kuwafikia wananchi wengi zaidi mijini na vijijini,” amesema Mchengerwa.
Aidha, Waziri huyo amesema Serikali itaendelea kuboresha mifumo ya utoaji wa chanjo kwa kuhakikisha huduma hizo zinapatikana kwa urahisi katika vituo vya afya, zahanati na hospitali nchini kote ili kuongeza ulinzi dhidi ya magonjwa yanayozuilika kwa chanjo.
Ameeleza kuwa hatua hiyo ni sehemu ya mkakati mpana wa Serikali wa kuimarisha afya ya mama na mtoto pamoja na kupunguza vifo vinavyotokana na magonjwa ya kuambukiza ambayo yanaweza kuzuilika kupitia chanjo.
Mbali na hilo, Serikali imeendelea kuhamasisha wananchi kujitokeza kupata chanjo pamoja na kushiriki katika kampeni mbalimbali za afya zinazolenga kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa kinga na huduma za afya za msingi.
Wadau wa afya wameendelea kuipongeza Serikali kwa hatua hiyo wakieleza kuwa kuongezeka kwa kiwango cha chanjo kutasaidia kujenga jamii yenye afya bora na kupunguza mzigo wa magonjwa nchini.
Kwa mujibu wa wataalamu wa afya, utoaji wa chanjo kwa kiwango kikubwa ni moja ya njia muhimu za kudhibiti magonjwa hatari kwa watoto na jamii kwa ujumla, huku mafanikio hayo yakitajwa kuiweka Tanzania katika nafasi nzuri ya kuendelea kuboresha sekta ya afya na huduma za kinga.
.png)

Na Hassan Kimweri, WAF - Dodoma
Sekta ya afya nchini imepata mafanikio makubwa katika kipindi cha awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan yaliyoongeza upatikanaji wa huduma za afya kwa wananchi kupitia ujenzi wa miundombinu, ununuzi wa vifaa tiba, uoatikanaji wa dawa pamoja na huduma za kibingwa na za dharura nchini.
Waziri wa Afya Mhe. Mohamed Mchengerwa amesema hayo leo Mei 11, 2026 wakati akiwasilisha Bajeti ya Wizara ya Afya kwa mwaka wa fedha 2026/27 katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya Spika wa Bunge Mhe. Mussa Azan Zungu.
"Eneo la vituo vya kutolea huduma za afya vimeongezeka kutoka elfu 10,153 mwaka 2021/22 hadi elfu 13,683 kufikia Machi 2026, sawa na ongezeko la vituo 3,530, Zahanati zimeongezeka kutoka elfu 7,189 hadi elfu 8,706 huku hospitali zikiongezeka kutoka mia 404 hadi mia 475 mwaka 2026," amesema Waziri Mchengerwa
Aidha, Waziri Mchengerwa amesema Serikali imeongeza majengo mapya katika hospitali mbalimbali zikiwemo Hospitali ya Muhimbili, KCMC, BMH, Bugando, Mirembe, pamoja na Kibong'oto huku ikiwa imejenga hospitali mpya 10 za rufaa za mikoa, kukarabati hospitali kongwe 50, kukamilisha maboma 980 ya zahanati na kujenga vituo vya afya 390.
Amesema, katika huduma za afya ya uzazi, mama na mtoto, Serikali imeongeza wodi za watoto wachanga kutoka 80 hadi 438 pamoja na vituo vya upasuaji wa dharura kutoka 445 hadi 630 ambayo ni mafanikio yaliyochangia kupungua kwa vifo vitokanavyo na uzazi kutoka vifo 556 mwaka 2016 hadi vifo 104 mwaka 2022 kwa kila vizazi hai 100,000.
"Katika huduma za uchunguzi na matibabu ya kibingwa, Serikali imenunua na kusimika vifaa tiba vyenye thamani ya Shilingi bilioni 241.6 ambapo mashine za MRI zimeongezeka kutoka 7 hadi 13, CT Scan kutoka 12 hadi 45 pamoja na Digital X-ray kutoka 147 hadi 559," amesema Waziri Mchengerea
Kwa upande wa chanjo, amesema watoto waliopata chanjo ya Pentavalent dozi ya tatu wameongezeka kutoka watoto milioni 2,093,412 hadi milioni 3,186,979 huku kiwango cha chanjo kikiongezeka kutoka asilimia 93 hadi 96, juu ya lengo la kimataifa la asilimia 90.
"Upatikanaji wa dawa na bidhaa za afya umeimarika, Serikali imetoa Shilingi trilioni 1.4 kwa ajili ya ununuzi wa dawa na vifaa tiba, viwanda vipya 11 vya dawa na vifaa tiba vimeanzishwa huku 'Tanzania Pharmaceutical Industries kikifufuliwa kwa ajili ya uzalishaji wa dawa za VVU nchini," amesema Waziri Mchengerea
Na Grace Michael, NHIF-Dodoma
Serikali imeanza rasmi utekelezaji wa Mpango wa Bima ya Afya kwa Wote kwa kaya zisizo na uwezo kwa kutoa Shilingi bilioni 48.8 kwa ajili ya kuwawezesha wananchi wa makundi maalum kupata huduma za afya kwa uhakika.
Kupitia utekelezaji huo, jumla ya kaya 172,297 tayari zimefikiwa na kuingizwa kwenye mpango huo, huku wanufaika 463,228 wakianza kupata huduma mbalimbali za matibabu katika vituo vilivyosajiliwa nchini.
Akiwasilisha Hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Afya Fungu 52 kwa mwaka 2026/27 Waziri wa Afya Mhe. Omary Mchengerwa amesema kuwa, utekelezaji huu unaonesha dhamira ya Serikali ya kuhakikisha kila Mtanzania anapata huduma bora za afya bila kujali hali yake ya kiuchumi, ikiwa ni sehemu ya safari ya kuelekea huduma jumuishi za afya kwa wananchi wote.
Katika kuimarisha sekta ya afya sambamba na utekelezaji wa mpango huo, mabaraza na bodi za kitaaluma yameendelea kusimamia ubora wa huduma kwa kusajili wataalam wa afya 14,310, hatua inayoongeza nguvu kazi muhimu kwa utoaji wa huduma nchini.
Amesema kuwa kuhusu upatikanaji wa huduma za matibabu, jumla ya maduka ya dawa 330 yamesajiliwa pamoja na watarajali 3,004, huku vituo vya kutolea huduma za afya 3,643 vikisajiliwa ili kuongeza upatikanaji wa huduma karibu na wananchi.
Katika kuhakikisha taaluma na maadili yanaendelea kuzingatiwa hususan wakati huu wa kuhudumia wananchi wengi zaidi kupitia mfumo wa Bima ya Afya, vituo binafsi vya afya 654 vimekaguliwa ili kuhakikisha vinakidhi viwango na kutoa huduma salama kwa wananchi.
Mafanikio hayo yanaakisi hatua kubwa ya Serikali katika kujenga mfumo imara wa afya unaojali usawa, ubora na upatikanaji wa huduma kwa wote, huku Bima ya Afya kwa Wote ikiendelea kuwa nguzo muhimu ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi.
Na Janeth Raphael- MichuziTv -Dodoma.
Mbunge wa Kigoma Mjini, Clayton Chipando maarufu kama Baba Levo, ameibua wasiwasi kuhusu kuendelea kwa migogoro ya ardhi nchini, akisema suala hilo limekuwa chanzo kikubwa cha migongano katika jamii kutokana na umuhimu mkubwa wa ardhi katika maisha ya watu.
Akizungumza bungeni, mbunge huyo amesema duniani kuna mambo matatu ambayo watu hupambana nayo kwa nguvu zote ambayo ni fedha, mapenzi na ardhi, akisisitiza kuwa migogoro mingi inayojitokeza nchini inahusishwa moja kwa moja na matumizi ya ardhi pamoja na mabadiliko ya matumizi ya maeneo yaliyotengwa kwa matumizi ya umma.
Mbunge huyo alihoji ni lini Serikali itaweka sheria kali zaidi zitakazodhibiti tabia ya kubadilisha matumizi ya maeneo ya wazi pamoja na maeneo yaliyotengwa kwa huduma za jamii, hali ambayo imekuwa ikichochea migogoro ya mara kwa mara katika maeneo mbalimbali nchini.
“Ardhi imekuwa chanzo kikubwa cha migogoro. Tunaona maeneo ya wazi na yale yaliyotengwa kwa matumizi ya umma yakibadilishwa matumizi kila mara. Serikali ina mpango gani wa kuweka sheria kali kudhibiti hali hii?” alihoji Baba Levo.
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Kaspar Mmuya, alisema Serikali inaendelea kuchukua hatua dhidi ya wote wanaovamia maeneo ya wazi au kuendeleza shughuli za ujenzi bila kufuata sheria, taratibu na mipango ya matumizi ya ardhi iliyowekwa.
Mmuya ametoa onyo kali kwa wananchi wanaojihusisha na ujenzi katika maeneo yaliyotengwa kwa matumizi ya umma bila kibali halali, akisema Serikali haitasita kubomoa majengo yote yaliyojengwa kinyume cha sheria bila kujali gharama zilizotumika katika ujenzi huo.
Alisisitiza kuwa ulinzi wa maeneo ya wazi ni muhimu kwa maendeleo ya miji na ustawi wa jamii, hivyo wananchi wanapaswa kufuata sheria za mipango miji na matumizi bora ya ardhi ili kuepusha migogoro isiyo ya lazima.
Aidha, Serikali imewahimiza wananchi kuhakikisha wanapata vibali na kufuata utaratibu sahihi kabla ya kuanza maendeleo yoyote ya ujenzi ili kulinda maeneo yaliyotengwa kwa manufaa ya umma pamoja na kudumisha utaratibu wa mipango miji nchini.






.jpeg)








.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)



.jpeg)


.jpeg)
.jpeg)


.jpeg)

.jpeg)




.jpeg)
