


MichuziBlogV2
Most read Swahili blog on earth
Bonyeza play kuangalia Michuzi TV LiVE
BONYEZA PLAY KUANGALIA AZAM TV LIVE
BONYEZA KUANGALIA CHANNEL TEN LIVE



Julai 1, 2026 Mhe. Dkt.Samia Suluhu Hassan , Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania atatoa Ramsi Tuzo ya Mlipakodi bora kwa walipakodi waliokidhi vigezo ili kuleta Hamasa ya ulipaji kodi nchini na kuwashukuru kwa mchango wao mkubwa katika maendeleo ya nchi yetu.
Sambamba na hilo TRA itaadhimisha miaka 30 tangu kuanzishwa kwake Julai 1 1996 ikisherehekea mahusiano mazuri yaliyo jengwa kati ya TRA na walipakodi kwa miongo mitatu na kuchangia maendeleo ya kila sekta katika nchi yetu. TRA inawashukuru sana walipakodi wote kwa kuendelea kulipa kodi kwa hiyari na kwa wakati kwa kipindi chote cha miaka thelathini. Miaka 30 ya TRA kulipa kodi ni Uzalendi na Ushujaa kwa maendeleo na kujitegemea kwa Taifa letu.
Bw. Jared Awando (wa tatu kutoka kushoto), Mtendaji Mkuu wa ICEA LION General Insurance Tanzania, akiwa pamoja na washindi wa mashindano ya gofu ya ICEA LION King of the Course na viongozi wa ICEA LION Group mara baada ya hafla ya utoaji wa tuzo iliyofanyika jijini Arusha. Mashindano hayo, yaliyofanyika ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Bima, yalimshuhudia Karim Jamal akitwaa ubingwa wa jumla na kujishindia safari yenye udhamini kamili ya kuiwakilisha Tanzania katika fainali za King of the Course zitakazofanyika Mombasa, Kenya, mwezi Oktoba mwaka huu, pamoja na zawadi nyingine mbalimbali.Serikali kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), kwa ufadhili wa Green Climate Fund (GCF), kwa kushirikiana na Shirika la Mazingira la Umoja wa Mataifa (UNEP) na Taasisi ya Utafiti wa Misitu Tanzania (TAFORI), imefikia hatua muhimu katika utekelezaji wa Mradi wa Kujenga Uhimilivu dhidi ya Athari za Mabadiliko ya Tabianchi katika Mkoa wa Kigoma kwa kuanza uthibitishaji wa matokeo ya tathmini ya awali (Baseline Survey) ya mradi huo kabla ya kuanza kwa zoezi muhimu la Mpango wa Matumizi Bora ya Ardhi kwa vijiji 22 vilivyopo katika wilaya za Kasulu, Kakonko na Kibondo.
Uthibitishaji huo unafanyika kupitia warsha inayofanyika katika Wilaya ya Kibondo, Mkoa wa Kigoma, na unalenga kuhakiki hali halisi ya kijamii, kiuchumi na kimazingira katika maeneo ya mradi kabla ya utekelezaji wa shughuli mbalimbali za kuimarisha uhimilivu wa jamii dhidi ya mabadiliko ya tabianchi.
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa warsha hiyo, Meneja wa Mradi kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira, Mhandisi Onesphory Kamukuru, alisema mradi unatekelezwa katika wilaya za Kasulu, Kibondo na Kakonko kutokana na maeneo hayo kuathiriwa kwa kiwango kikubwa na uharibifu wa mazingira, mmomonyoko wa ardhi na athari nyingine za mabadiliko ya tabianchi.
Alieleza kuwa mojawapo ya sababu zilizochangia uharibifu huo ni historia ya maeneo hayo kupokea idadi kubwa ya wakimbizi, hali iliyosababisha ongezeko la matumizi ya rasilimali za misitu, ikiwemo ukataji wa miti kwa ajili ya kuni na mkaa.
“Mradi huu ni wa wananchi na unatekelezwa katika maeneo matatu makuu ambayo ni kilimo mseto, usimamizi wa hifadhi za misitu ya vijiji na za TFS pamoja na kurejesha maeneo yaliyoharibiwa na mmomonyoko wa ardhi,” alisema Mhandisi Kamukuru.
Mradi huo unatekelezwa katika vijiji 22 vya wilaya za Kasulu, Kibondo na Kakonko, ambavyo vimeathiriwa kwa kiwango kikubwa na mabadiliko ya tabianchi na uharibifu wa mazingira, hususan vijiji vilivyo karibu na maeneo yaliyowahi kuhifadhi wakimbizi.
Katika mradi huu, TAFORI imepewa jukumu la kukusanya na kuchambua taarifa za awali zitakazotumika kama msingi wa ufuatiliaji na tathmini ya utekelezaji wa mradi. Aidha, taasisi hiyo inasimamia utekelezaji wa shughuli za kitaalamu katika maeneo matatu ya kipaumbele ambayo ni Usimamizi Shirikishi wa Misitu ya Jamii (CBFM), Kilimo Mseto (Agroforestry) na Upandaji Miti (Afforestation).
Akizungumza kwa niaba ya timu ya wataalamu wa TAFORI, Mtafiti Mwandamizi na Msimamizi wa Ushauri wa Kitaalamu wa Mradi, Dkt. Numan Amanzi, alisema matokeo ya tathmini ya awali yaliyowasilishwa kwa wadau yameridhisha na yanaakisi hali halisi iliyopo katika vijiji vinavyotekeleza mradi.
“Matokeo haya yatatumika kama msingi wa kupima mafanikio ya mradi baada ya kukamilika ili kubaini kwa kiwango gani umechangia kuboresha hali za kiuchumi, kijamii na kimazingira katika jamii husika,” alisema Dkt. Amanzi.
Hatua ya uthibitishaji wa matokeo ya tathmini ya awali ni awamu ya tatu ya utekelezaji wa mradi. Awamu ya kwanza ilihusisha utambulisho wa mradi kwa mamlaka za Mkoa wa Kigoma na wilaya husika, huku awamu ya pili ikihusisha uthibitishaji wa vigezo vya uteuzi wa vijiji, maeneo ya utekelezaji na aina za miti zitakazotumika katika shughuli za usimamizi shirikishi wa misitu, kilimo mseto na upandaji miti.
Warsha hiyo imewakutanisha wadau mbalimbali wakiwemo wawakilishi kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, Maafisa Mazingira, Maafisa Mkoa, Wilaya na Wakala wa Huduma za Misitu (TFS) na Wawakilishi wa vijiji 22 vya wilaya za Kasulu, kibondo na Kakonko.

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dkt. Leonard Akwilapo, amesema Serikali itaendelea kushirikiana kwa karibu na taasisi za kidini katika kuboresha huduma za jamii, hususan sekta za elimu, afya na malezi, kwa kutambua mchango mkubwa wa taasisi hizo katika maendeleo ya taifa.
Dkt. Akwilapo ameyasema hayo Juni 28, 2026, mkoani Dodoma aliposhiriki Harambee ya Ujenzi wa Nyumba za Walimu katika Shule ya St. Peters and St. Paul Secondary School iliyopo Wilaya ya Kondoa. Hafla hiyo ilihudhuriwa pia na Baba Askofu wa Kanisa la Anglikana Dayosisi ya Kondoa, Askofu Given Gaula, pamoja na viongozi na waumini wa kanisa hilo.
Katika hafla hiyo, Waziri huyo alishiriki pia ibada maalumu ya kumsimika mfadhili kutoka Uingereza, Bw. Peter Ruxton, kuwa Lay Canon wa Kanisa la Anglikana Dayosisi ya Kondoa kutokana na mchango wake mkubwa katika maendeleo ya elimu na shughuli za kanisa.
Akizungumza katika hafla hiyo, Dkt. Akwilapo alisema Serikali inaendelea kutekeleza maelekezo ya Rais ya kuimarisha ushirikiano na madhehebu mbalimbali ya dini kwa lengo la kuboresha huduma za jamii zinazowagusa wananchi moja kwa moja.
"Rais amekuwa akituambia kuwa ataendelea kushirikiana na madhehebu ya dini, na azma yake ni kuboresha huduma za jamii," alisema Dkt. Akwilapo.
Alisema Serikali inatambua mchango mkubwa wa Kanisa la Anglikana katika sekta ya elimu, akibainisha kuwa kwa mujibu wa takwimu za Wizara ya Elimu, kanisa hilo linaendesha shule za awali 39, shule za msingi 40, shule za sekondari 17, vyuo vya kati 17 pamoja na chuo kikuu kimoja.
Alieleza kuwa taasisi hizo zimeendelea kutoa mchango muhimu katika kuwajengea vijana maarifa, maadili, uzalendo na hofu ya Mungu, mambo ambayo ni msingi wa maendeleo endelevu ya taifa.
Aidha, Dkt. Akwilapo aliipongeza Dayosisi ya Kondoa kwa juhudi zake za kupanua huduma za elimu kwa kuongeza idadi ya shule, akieleza kuwa hivi karibuni shule nyingine itazinduliwa katika wilaya hiyo.
Kwa upande wake, Askofu wa Kanisa la Anglikana Dayosisi ya Kondoa, Dkt Given Gaula, amesema ili kumtia moyo mfadhili anayesaidia maendeleo ya kanisa ikiwemo ujenzi wa shule waumini wa kanisa hilo wanapaswa kuchanga fedha kwa ajili ya maendeleo ya ujenzi wa nyumba za walimu.
‘’Shule zinazoendeshwa na kanisa la Angilikana hapa Kondoa zimeleta mabadiliko makubwa katika maisha ya watoto kwa kutoa elimu bora bila ubaguzi wa dini au itikadi’’. amesema
Jumla ya shilingi milioni tano zilichangwa katika hafla hiyo ikiwa ni jitihada za kumuunga mkono mfadhili anayejenga nyumba za walimu katika Shule za St. Peters and St. Paul Secondary School iliyopo Wilaya ya Kondoa
Katika hatua nyingine, Dkt. Akwilapo alimpongeza Bw. Peter Ruxton baada ya kusimikwa kuwa Lay Canon, akisema ametoa mchango wa kipekee katika maendeleo ya elimu na shughuli za kanisa kwa miaka mingi.
Alisema Serikali inathamini mchango wa mfadhili huyo, ambaye amesaidia kujenga na kuendeleza shule mbalimbali pamoja na kuchangia maendeleo ya taasisi za kidini zinazotoa huduma kwa jamii bila ubaguzi.
Naye Askofu Dkt Given Gaula alisema Bw. Ruxton amekuwa mshirika muhimu wa Dayosisi ya Kondoa, akibainisha kuwa karibu asilimia 97 ya shule zinazomilikiwa na dayosisi hiyo zimejengwa kwa msaada wake.
Aidha, amesema mfadhili huyo amechangia ununuzi wa mabati kwa makanisa mengi yaliyopo vijijini na kusaidia miradi mingine ya maendeleo inayowanufaisha wananchi.
Alisisitiza kuwa ushirikiano kati ya Serikali, taasisi za kidini na wadau wa maendeleo unaendelea kuwa chachu muhimu katika kuimarisha elimu, kuboresha ustawi wa jamii na kuharakisha maendeleo ya taifa.
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dkt. Leonard Akwilapo akizungumza wakati wa Harambee ya Ujenzi wa Nyumba za Walimu katika Shule ya St. Peters and St. Paul Secondary School iliyopo Wilaya ya Kondoa jana.
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dkt. Leonard Akwilapo akishiriki ibada wakati wa Harambee ya Ujenzi wa Nyumba za Walimu katika Shule ya St. Peters and St. Paul Secondary School iliyopo Wilaya ya Kondoa tarehe 28 Julai 2026.
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dkt. Leonard Akwilapo akipongezwa alipopatiwa zawadi mara baada ya kuendesha Harambee ya Ujenzi wa Nyumba za Walimu katika Shule ya St. Peters and St. Paul Secondary School iliyopo Wilaya ya Kondoa.