Serikali imeahidi kuhakikisha washiriki wa mafunzo ya ujasiriamali yanayotolewa na Jukwaa Huru la Wahariri Tanzania (JUWATA) wanayafanyia kazi kwa vitendo kwa kuwawezesha katika mikopo inayotolewa na Halmashauri kupitia utengenezaji wa bidhaa mbalimbali zitakazochangia ukuaji wa uchumi.

Kauli hiyo imetolewa mkoani Morogoro na Katibu Tawala Msaidizi Sehemu ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Beatrice Njawa, wakati akifungua mafunzo hayo kwa wananchi.

Bi.Njawa ambaye katika semina hiyo alimwakilisha Mgeni Rasmi, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Adam Malima amesema Serikali inataka kuona mafunzo hayo yanazaa matokeo ya moja kwa moja kwa washiriki kuanzisha na kuendeleza viwanda vidogo, kusindika mazao ya kilimo na kutengeneza bidhaa zenye ubora wa kushindana sokoni.

Mafunzo hayo ya siku tatu yanayoratibiwa na Jukwaa huru la Wahariri Tanzania (JUWATA) na kutolewa na wakufunzi wa taasisi ya MAMO ENTREPRNEURSHIP yanalenga kuwajengea wananchi mbalimbali uwezo wa kubuni miradi ya ujasiriamali itakayowaongezea kipato na kuchangia ajira kwa vijana.

Mbali na hayo Njawa amelipongeza JUWATA kwa kuona mbali na kuunga mkono juhudi za Serikali za kujenga uchumi wa viwanda. “Habari peke yake haitoshi. Amesema kuwa Mwandishi wa habari anaweza kuwa mtengenezaji wa bidhaa na mtumishi wa umma anaweza kuwa mjasiriamali huo ndio mwelekeo wa taifa,” amesema Bi.Njawa.

Katika hatua nyingine Bi.Njawa ameeleza kuwa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Morogoro kupitia Sehemu ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji itafanya ufuatiliaji wa karibu kuhakikisha washiriki wanatekeleza waliyojifunza na kuahidi kuwa vikundi vitakavyofanya vizuri vitapewa kipaumbele na mwakani 2027 watapelekwa katika maonesho ya Sabasaba.

Mafunzo hayo ni sehemu ya mkakati wa JUWATA wa kuwajengea wanachama wake uwezo wa kujitegemea kiuchumi sambamba na kutekeleza majukumu yao ya kuhabarisha umma.
















Na Janeth Raphael - MichuziTv 

Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Carolyne Nombo, ametoa maagizo matano kwa viongozi na watumishi wa sekta ya elimu nchini yenye lengo la kuimarisha ubora wa elimu na kuhakikisha sekta hiyo inaendana na mahitaji ya maendeleo ya taifa pamoja na mabadiliko ya dunia.

Profesa Nombo ametoa maagizo hayo wakati akifungua Kikao cha Mwaka cha Menejimenti ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia pamoja na Wakuu wa Taasisi zilizo chini ya Wizara hiyo, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda.

Akizungumza katika kikao hicho, amesema mafanikio makubwa yaliyopatikana katika sekta ya elimu yametokana na ushirikiano, uwajibikaji na utendaji mzuri wa viongozi na watumishi wa wizara pamoja na taasisi zake.

Ameeleza kuwa kikao hicho ni jukwaa muhimu la kufanya tathmini ya utekelezaji wa majukumu ya sekta ya elimu na kuweka mikakati itakayoiwezesha sekta hiyo kuchangia kikamilifu utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

“Tumewaalika wataalamu kutoka Tume ya Mipango ili kwa pamoja tuangalie namna sekta ya elimu itakavyotoa mchango wake katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050. Dira hiyo ndiyo itakayoongoza maendeleo ya taifa kwa miongo ijayo,” alisema Profesa Nombo.

Katika maagizo yake, Profesa Nombo alisisitiza umuhimu wa kufanya mapitio ya mara kwa mara ya kozi na programu za elimu ili ziendane na mahitaji ya sasa ya jamii, uchumi na soko la ajira.

Amesema mjadala unaoendelea katika mitandao ya kijamii kuhusu kozi zinazopaswa kusomwa na wahitimu wa kidato cha sita umeonesha wazi kuwa kuna mahitaji mapya ya ujuzi na taaluma zinazotakiwa katika soko la ajira la sasa na la baadaye.

“Mrejesho tunaoupata unatufanya tujitathmini na kuangalia kama kozi tunazotoa zinakidhi mahitaji halisi ya maendeleo ya taifa. Tunapaswa kuongeza ubunifu na unyumbufu ili wanafunzi wapate fursa ya kusoma taaluma zinazohitajika zaidi,” alisema.

Aidha, ameagiza taasisi zote zilizo chini ya wizara kuhakikisha zinaunganisha mifumo yao ya TEHAMA na Mfumo wa Taarifa za Usimamizi wa Elimu (ESMIS), akisisitiza kuwa uwepo wa takwimu sahihi ni msingi wa kufanya maamuzi yenye tija na kuboresha utoaji wa huduma.

Amesema hatua hiyo inatekeleza maelekezo ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha mifumo ya Serikali inasomana na kufanya kazi kwa pamoja ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma kwa wananchi.

Profesa Nombo pia alihimiza kuimarishwa kwa ushiriki wa sekta binafsi katika uwekezaji wa elimu ili kuboresha miundombinu, kuongeza ubora wa huduma na kupanua fursa za elimu kwa Watanzania wengi zaidi.

Vilevile, alisisitiza umuhimu wa kutafuta vyanzo mbadala vya kugharamia sekta ya elimu ili kuwezesha wanafunzi wengi zaidi kuendelea na masomo yao bila vikwazo vya kifedha.

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Daniel Mushi, aliwataka viongozi na watendaji wa sekta hiyo kuendelea kueleza kwa wananchi mafanikio yanayopatikana kupitia utekelezaji wa miradi na programu mbalimbali za Serikali.

“Tusisite kueleza mafanikio yanayopatikana kutokana na uwekezaji wa Serikali katika sekta ya elimu. Kwa kufanya hivyo, tunajenga uelewa wa wananchi na kuendelea kuimarisha sekta ya elimu yenye ushindani na tija kwa maendeleo ya taifa,” alisema Profesa Mushi.

Katika kikao hicho, washiriki walipokea na kujadili mawasilisho mbalimbali yaliyohusu mchango wa elimu, sayansi na teknolojia katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, matumizi ya mifumo ya TEHAMA na ESMIS katika kuongeza ufanisi wa utoaji wa huduma, pamoja na Mpango Mkakati wa Wizara wa mwaka 2026/27 hadi 2030/31 na utekelezaji wa Bajeti ya mwaka 2026/27.






Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa, ameitaka Bodi mpya ya pili ya Shirika la Uvuvi Tanzania (TAFICO) kuhakikisha uwekezaji mkubwa uliofanywa na Serikali katika sekta ya uvuvi unatafsiriwa kuwa uzalishaji wa kibiashara, mapato na mchango mkubwa zaidi katika uchumi wa Taifa.

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa bodi hiyo iliyofanyika Julai 13, 2026, katika Ofisi za Makao Makuu ya TAFICO, Ras Mkwavi, Kigamboni jijini Dar es Salaam, Waziri Dkt. Bashiru alisema Bodi hiyo inaanza kazi katika kipindi muhimu ambacho Serikali imeweka msisitizo mkubwa katika kukuza uchumi wa buluu kupitia uwekezaji wa kimkakati kwenye sekta ya uvuvi ikiwa ni utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050.

"Mnaanza kazi wakati ambao msingi wa uwekezaji umeanza kujengwa. Hivyo jukumu lenu ni kuhakikisha uwekezaji huo unazaa matokeo chanya ya kibiashara na ya maendeleo kwa Taifa," alisema Dkt. Bashiru.

Katika maelekezo yake, Waziri aliitaka Bodi kusimamia kwa karibu ukamilishaji wa miradi ya kimkakati ikiwemo uendeshaji wa meli ya uvuvi wa bahari kuu kwa utaratibu wa ubia (PPP), kuharakisha mabadiliko ya TAFICO kutoka hatua ya maandalizi kwenda uzalishaji halisi wa kibiashara, kupitia upya mpango mkakati na maandiko ya uwekezaji, kuimarisha upatikanaji wa rasilimali fedha, kujenga rasilimali watu yenye uwezo, kufanya maboresho ya muundo wa Shirika, kuendeleza ushirikiano na sekta binafsi pamoja na kuhakikisha uwazi, uwajibikaji na usimamizi wa mali zote za Shirika.

Akizungumza kwa niaba ya Bodi ya Wakurugenzi, Mwenyekiti wa Bodi ya TAFICO Prof. Yunus Daud Mgaya, aliishukuru Serikali kwa kuiamini Bodi hiyo kuiongoza TAFICO katika kipindi cha miaka mitatu, akiahidi kuwa Bodi itafanya kazi kwa weledi, uwajibikaji na ushirikiano wa karibu na Wizara pamoja na Menejimenti ili kuhakikisha maelekezo yaliyotolewa na Waziri yanatekelezwa kikamilifu

Awali akizungumza kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo anayeshughulikia sekta ya uvuvi, Prof. Mohammed Sheikh, alisema sekta ya uvuvi inaendelea kuwa miongoni mwa sekta zenye mchango mkubwa katika maendeleo ya uchumi wa Taifa, huku Serikali ikiendelea kuwekeza katika miradi ya kimkakati ikiwemo Bandari ya Uvuvi ya Kilwa Masoko na kuimarisha Shirika la Uvuvi Tanzania (TAFICO) ili liwe chombo kikuu cha kuendesha uvuvi wa kibiashara nchini.

Kwa upande wake, Afisa Mtendaji Mkuu wa TAFICO, CPA Shaibu Matessa, alisema Shirika limeingia katika hatua mpya ya maendeleo ambapo linaendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya kimkakati inayolenga kuifanya TAFICO kuwa taasisi ya kisasa ya kibiashara katika sekta ya uvuvi.

Uzinduzi wa Bodi ya Pili ya Wakurugenzi wa TAFICO unatarajiwa kuwa chachu ya kuimarisha usimamizi wa uwekezaji wa Serikali katika sekta ya uvuvi na kuhakikisha Shirika linafikia dhamira ya kuwa nguzo ya utekelezaji wa ajenda ya uchumi wa buluu kupitia uzalishaji, biashara na uendelezaji wa rasilimali za uvuvi kwa manufaa ya Taifa.

Sanjari na tukio hilo, Waziri Dkt. Bashiru amezindua maandalizi ya Kongamano la Kimataifa la Ukuzaji Viumbemaji Duniani (WA26T) na Ukuzaji Viumbemaji Afrika (AFRAQ26), ambapo Tanzania itakuwa mwenyeji wa Kongamano hilo litakalofanyika Desemba,2026 Jijini Dar es salaam.
Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa (kulia), akimkabidhi nyaraka za Utendaji kazi Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya TAFICO Prof. Yunus Daud Mgaya, katika Hafla ya Uzinduzi wa Bodi hiyo iliyofanyika Julai 13, 2026, katika Ofisi za Makao Makuu ya TAFICO, Ras Mkwavi, Kigamboni jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Dkt. Bashiru Ally Kakurwa kizungumza wakati akizindua Bodi ya pili ya Wakurugenzi ya TAFICO, katika hafla ya uzinduzi iliyofanyika Julai 13, 2026, katika Ofisi za Makao Makuu ya TAFICO, Ras Mkwavi, Kigamboni jijini Dar es Salaam.
Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya TAFICO Prof. Yunus Daud Mgaya akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi wa Bodi mpya ya pili ya Shirika la Uvuvi Tanzania (TAFICO) uliyofanyika, katika Ofisi za Makao Makuu ya TAFICO, Ras Mkwavi, Kigamboni jijini Dar es Salaam.
Afisa Mtendaji Mkuu wa Shirika la Uvuvi Tanzania (TAFICO) CPA Shaibu Matessa, akizungumza wakati wa uzinduzi wa Bodi ya pili ya Wakurugenzi ya TAFICO, katika hafla ya uzinduzi iliyofanyika Julai 13, 2026, katika Ofisi za Makao Makuu ya TAFICO, Ras Mkwavi, Kigamboni jijini Dar es Salaam.
Mkutano ukiendelea
Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa (walioketi katikati), akiwa kwenye picha ya pamoja na wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi ya TAFICO, katika Hafla ya Uzinduzi wa Bodi hiyo iliyofanyika Julai 13, 2026, katika Ofisi za Makao Makuu ya TAFICO, Ras Mkwavi, Kigamboni jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA), Mha. Wolta Kirita, amesisitiza umuhimu wa kushirikisha Vyombo vya Utoaji wa Huduma ya Maji Ngazi ya Jamii (CBWSOs) katika mipango na programu zote zinazolenga kuboresha huduma za maji vijijini ili kuhakikisha huduma hizo zinakuwa endelevu na wananchi wanaendelea kunufaika na uwekezaji mkubwa unaofanywa na Serikali.

Mha. Kirita ametoa maelekezo hayo Julai 13, 2026, wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya siku tatu kuhusu utekelezaji wa Programu ya Lipa kwa Matokeo (PforR II) Awamu ya Pili, yanayofanyika katika Ukumbi wa Rocky City Mall, jijini Mwanza. Mafunzo hayo yanawakutanisha waratibu wa programu kutoka Wizara za Maji, Afya, Elimu na TAMISEMI.

Akizungumza na Mameneja wa Mikoa (RMs) na Mameneja wa Wilaya (DMs), Mkurugenzi Mkuu aliwataka kuendelea kuzisimamia CBWSOs kwa ukaribu na kuhakikisha zinajengewa uwezo wa kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi. Alieleza kuwa RUWASA inaelekea kuanzisha mfumo wa mikataba ya utendaji kazi ili kuongeza uwajibikaji na kuondokana na utendaji wa mazoea (business as usual), kwa lengo la kujenga utamaduni wa matokeo.

«“RMs na DMs ninyi ndiyo DGs kwenye maeneo yenu. Mmepewa mamlaka ya kufanya maamuzi kwa niaba ya taasisi, hivyo yatumieni ipasavyo. Natamani kuona Makao Makuu yakijikita zaidi katika kazi za kimkakati, kama kutafuta programu mpya za maendeleo badala ya kushughulikia masuala ya kawaida ya usimamizi wa miradi,” alisema Mha. Kirita.»

Aidha, aliwataka viongozi hao kuendelea kuzisaidia CBWSOs kuandaa mipango bora ya uendeshaji na matengenezo, kuwajengea uwezo, kuhakikisha upatikanaji wa vipuri kupitia mfumo wa framework contracts, kuimarisha matengenezo kinga na kusimamia matumizi sahihi ya fedha ili kuhakikisha huduma za maji zinaendelea kuwa endelevu.

«“Uendelevu wa huduma za maji unategemea pia utunzaji wa vyanzo vya maji. Hili ni jukumu la kila mmoja wetu na tunapaswa kulisimamia kwa pamoja,” alisisitiza.»

Mkurugenzi Mkuu alisema muundo wa RUWASA umeendelea kuonesha ufanisi katika utoaji wa huduma za maji safi vijijini na kusisitiza kuwa wadau wote wanaotekeleza Programu ya PforR kutoka sekta mbalimbali wanapaswa kushirikiana kwa karibu ili kufanikisha malengo yaliyowekwa.

Alibainisha kuwa mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha miaka mitano ya Awamu ya Kwanza ya Programu ya PforR yanapaswa kuwa chachu ya kuongeza kasi ya utekelezaji katika Awamu ya Pili itakayoanza kutekelezwa katika mwaka wa fedha 2026/2027.

Katika kuimarisha uendelevu wa huduma za maji vijijini, RUWASA imeendelea kutekeleza mkakati wa kuzijengea uwezo CBWSOs kupitia ukaguzi wa utendaji, mafunzo ya uendeshaji na matengenezo, pamoja na usimamizi unaolenga kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.










 Watumishi Housing Investments (WHI) imeendelea kuthibitisha ubora wake katika sekta ya makazi baada ya kutwaa Tuzo ya Tatu ya Banda Bora kwenye Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), katika kipengele cha Wajenzi wa Makazi (Real Estate Exhibitor).

Ushindi huo unaifanya WHI kuandika rekodi ya kutwaa tuzo katika maonesho hayo kwa miaka mitano mfululizo, jambo linalodhihirisha ubunifu, ubora wa huduma na dhamira ya taasisi hiyo ya kuendelea kutoa suluhisho la makazi bora kwa Watanzania.

WHI imewashukuru wateja, wadau na wananchi wote waliotembelea banda lake katika Maonesho ya Sabasaba, ikiahidi kuendelea kubuni huduma na miradi ya makazi yenye viwango vya juu ili kukidhi mahitaji ya wananchi na kuchangia maendeleo ya sekta ya nyumba nchini.

Na Janeth Raphael - MichuziTv

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema mawakili na maafisa wa sheria wa Serikali wana nafasi ya msingi katika kulinda rasilimali za taifa kwa maamuzi yote ya Serikali yanaongozwa na sheria, weledi na uzalendo.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Chama cha Mawakili wa Serikali uliofanyika jijini Arusha leo, Rais Samia amesema taaluma ya sheria ni nyenzo muhimu ya kuzuia hasara kwa Serikali kupitia ushauri wa kitaalamu unaotolewa kabla ya maamuzi makubwa kufanyika.

Ameeleza kuwa mwanasheria mwenye weledi anaweza kusaidia kulinda mikataba ya Serikali, kuimarisha uwajibikaji na kuhakikisha rasilimali za umma zinasimamiwa kwa manufaa ya wananchi. Kwa mujibu wake, jukumu hilo halihitaji nguvu za kijeshi, bali linahitaji uadilifu, uzalendo na uamuzi sahihi unaozingatia sheria.

Rais Samia pia amezitaka taasisi zote za umma kuimarisha mifumo ya kutambua mapema vihatarishi vya kisheria, hususan katika maeneo ya mikataba, manunuzi ya umma, ardhi, miradi ya maendeleo, TEHAMA, mazingira, ajira na utoaji wa huduma kwa wananchi.

Katika hatua nyingine, amesema Serikali inaendelea na mchakato wa kutafsiri sheria kwa lugha ya Kiswahili ili kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu haki zao, wajibu wao na mipaka ya mamlaka ya Serikali, jambo litakalosaidia kuimarisha utawala wa sheria nchini.

Aidha, Rais amesema mawakili wa Serikali wana mchango mkubwa katika kufanikisha utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050, akibainisha kuwa maeneo kama uchumi wa kidijitali, ulinzi wa taarifa binafsi, usimamizi wa rasilimali, ubia kati ya sekta ya umma na binafsi pamoja na biashara za kikanda yanahitaji mifumo madhubuti ya sheria na taasisi zenye uwajibikaji.

Amehitimisha kwa kusisitiza kuwa Serikali itaendelea kulinda haki za binadamu kwa kuzingatia Katiba na sheria za nchi, huku akiwataka mawakili wa Serikali kuhakikisha sheria wanazosimamia zinaendelea kulinda haki za wananchi, kuimarisha utawala wa sheria na kuhifadhi maslahi ya taifa katika mazingira yanayoendelea kubadilika duniani.





Na Janeth Raphael - Michuzi Tv 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema mafanikio ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 yatategemea uwepo wa mfumo madhubuti wa sheria unaolinda maslahi ya nchi, kuimarisha utoaji wa haki na kuweka mazingira rafiki ya ukuaji wa uchumi unaoendeshwa na maarifa, ubunifu na uwekezaji.

Akifungua Mkutano Mkuu wa Chama cha Mawakili wa Serikali uliofanyika jijini Arusha leo, Rais Samia amesema wataalamu wa sheria wana jukumu kubwa la kuhakikisha mfumo wa kisheria unaendana na kasi ya maendeleo na mahitaji mapya ya taifa katika kipindi cha miaka 25 ijayo.

Ameeleza kuwa Tanzania inapoelekea kutekeleza Dira ya 2050, maeneo kama uchumi wa kidijitali, ulinzi wa taarifa na data, usimamizi wa rasilimali za madini, ardhi na bandari, pamoja na biashara za kikanda na ubia kati ya sekta ya umma na binafsi, yanahitaji sheria bora, sera zinazotabirika na mikataba yenye tija ili kuongeza ushindani wa uchumi na kuvutia uwekezaji.

Rais Samia amesema mabadiliko yanayoendelea duniani katika nyanja za uchumi na siasa yanapaswa kuwa chachu kwa wataalamu wa sheria kuongeza umakini katika kulinda maslahi ya taifa, rasilimali zake na kuhakikisha mikataba yote inazingatia manufaa ya Watanzania.

Aidha, amewataka mawakili wa Serikali kuendelea kusimamia utungaji na utekelezaji wa sheria zinazolinda uhuru wa nchi, haki za wananchi na mali za umma, huku akizitaka taasisi za Serikali kuimarisha mifumo ya kutambua na kudhibiti vihatarishi vya kisheria katika mikataba, manunuzi ya umma, miradi ya maendeleo, ardhi, TEHAMA, mazingira na utoaji wa huduma.

Katika hatua nyingine, Rais Samia amesema Serikali inaendelea na mchakato wa kutafsiri sheria mbalimbali kwa lugha ya Kiswahili ili kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu haki na wajibu wao, hatua aliyoeleza kuwa itasaidia kuimarisha utawala wa sheria, uwajibikaji na ushiriki mpana wa wananchi katika maendeleo ya taifa.

Amesisitiza kuwa mfumo imara wa sheria si msingi wa utoaji wa haki pekee, bali pia ni nguzo muhimu ya maendeleo endelevu, ustawi wa uchumi na ulinzi wa maslahi ya Tanzania kwa vizazi vya sasa na vijavyo.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na viongozi, Mawakili, wageni mbalimbali, kabla ya kufungua Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Chama cha Mawakili wa Serikali Tanzania (TPBA) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC) Jijini Arusha tarehe 13 Julai, 2026.
Viongozi, wageni mbalimbali wakiwa kwenye ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Chama cha Mawakili wa Serikali (TPBA) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC) Jijini Arusha tarehe 13 Julai, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea zawadi ya nakala ya Kitabu cha Falsafa ya Sheria ya Mama Samia (Mama Samia Doctrine of Law); kutoka kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Hamza Johari kabla ya kufungua Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Chama cha Mawakili wa Serikali Tanzania (TPBA) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC) Jijini Arusha tarehe 13 Julai, 2026. Kitabu hicho kinaelezea historia, falsafa na mafanikio ya Tanzania chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia.
Picha namba 04. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea Tuzo ya Heshima kutoka kwa Rais wa Chama cha Mawakili wa Serikali Bw. Bavoo Anatoly Junus kabla ya kufungua Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Chama cha Mawakili wa Serikali Tanzania (TPBA) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC) Jijini Arusha tarehe 13 Julai, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea Tuzo ya Heshima kutoka kwa Rais wa Chama cha Mawakili wa Serikali Bw. Bavoo Anatoly Junus kabla ya kufungua Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Chama cha Mawakili wa Serikali Tanzania (TPBA) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC) Jijini Arusha tarehe 13 Julai, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akitembelea Mabanda ya maonesho ya masuala mbalimbali ya Sheria kabla ya kufungua Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Chama cha Mawakili wa Serikali Tanzania (TPBA) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC) Jijini Arusha, tarehe 13 Julai, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwasili katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC) kwa ajili ya kufungua Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Chama cha Mawakili wa Serikali Tanzania (TPBA) Jijini Arusha, tarehe 13 Julai, 2026.

Top News