Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Mambo ya Ndani ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Bw. Shaibu Mmari, amesema ushirikiano kati ya TRA na mawakala wa forodha ni nguzo muhimu katika kuimarisha usimamizi wa maadili na uwajibikaji kwa watumishi wa Mamlaka.

Bw. Mmari amesema hayo jijini Dar es Salaam wakati wa kikao cha mazungumzo kati ya TRA na viongozi wa Chama cha Waondoshaji na Wapelekaji Shehena Bandarini na Mipakani Tanzania (TAFFA), kilicholenga kuimarisha mahusiano ya kikazi na kubadilishana taarifa kuhusu uvunjifu wa maadili unaoweza kujitokeza katika shughuli za forodha.

Amesema kuwa ushirikiano wa karibu kati ya TRA na wadau wa sekta ya forodha ni muhimu katika kusaidia kubaini na kudhibiti vitendo vinavyokiuka maadili, pamoja na kuimarisha uwazi na uwajibikaji katika utoaji wa huduma.

“TRA ina jukumu la kukusanya mapato ya Serikali, kusimamia shughuli za forodha, na kuhakikisha sheria na taratibu za ushuru zinafuatwa ipasavyo. Ushirikiano na wadau kama TAFFA unatusaidia kuimarisha uadilifu na kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu haya,” amesema Bw. Mmari.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa wadau kuendelea kushirikiana na TRA katika kutoa taarifa pale wanapoona dalili za uvunjifu wa maadili au vitendo vinavyoweza kuathiri uadilifu wa huduma za forodha.

Kwa upande wake, Mhasibu Mkuu wa TAFFA, Bw. Anthony Mukyamuzi, ameipongeza TRA kwa juhudi inazoendelea kufanya katika kuboresha mifumo ya forodha na utoaji wa huduma kwa wadau.

Amesema maboresho hayo yameongeza ufanisi katika shughuli za uondoshaji na uingizaji wa mizigo bandarini na mipakani, na kuimarisha mazingira ya biashara kwa wadau wa sekta ya usafirishaji na uondoshaji shehena.

Mwisho, pande hizo mbili zimeahidi kuendelea kuimarisha ushirikiano katika kubadilishana taarifa, kuhamasisha maadili mema kwa watumishi, na kujenga mfumo wa uwajibikaji utakaosaidia kulinda uadilifu wa shughuli za forodha nchini.

 

Watanzania SABA waliokuwa nchini Iran wamewasili jijini Dar es Salaam Machi 13, 2026, kufuatia operesheni ya uokozi iliyoratibiwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Watanzania hao wamewasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) saa 8:40 usiku kwa kutumia Shirika la Ndege la Uturuki, wakitokea nchini Uturuki ambako walipokewa awali baada ya kuvuka mpaka wa nchi kavu wakitokea nchini Iran.

Katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere (JNIA) Watanzania hao walipokelewa na Mkurugenzi wa Idara ya Mashariki ya Kati kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Abdallah Kilima na maafisa wengine wa Wizara.

Mapokezi ya Watanzania hao yaligubikwa na hisia za faraja kutoka kwa ndugu na jamaa waliokuwa na hofu kubwa juu ya hatima ya usalama wa wapendwa wao.

Wakizungumza baada ya kuwasili uwanjani hapo Watanzania hao wameishukuru Serikali kwa kuratibu suala la kurejeshwa kwak nchini kwani imekuwa ni faraja kubwa kwao kurudi nyumbani salama kutokana na machafuko yanayoendelea nchini iran.

Serikali ya Tanzania ilichukua hatua za dharura kulinda maisha ya raia wake waliokuwa nchini humo kwa masomo na shughuli nyingine.

Safari ya kurejea nyumbani kwa Watanzania hao ilianzia kwenye mpaka wa Razi (Iran) na kufika Kapıkule (Uturuki) mnamo Machi 11, 2026 na kupokelewa na Balozi wa Tanzania Uturuki Mheshimiwa Iddi Seif Bakari na maafisa wa Ubalozi wa Tanzania nchini humo.

Serikali ya Tanzania ilichukua hatua za dharura kuokoa maisha ya raia wake waliokuwa nchini Iran kwa masomo na shughuli nyingine.

Watanzania hao waliorejea nyumbani wana hali nzuri kiafya na Serikali itaendelea kufuatilia kwa karibu hali ya usalama katika ukanda wa nchi za Ghuba ili kuhakikisha Watanzania wengine waliosalia katika nchi hizo wanakuwa salama.






Kwa niaba ya Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira (TRAMEPRO), napenda kuungana na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na jumuiya ya kimataifa katika kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Figo. Siku hii ni muhimu katika kuongeza uelewa wa jamii kuhusu umuhimu wa kulinda na kutunza afya ya figo.

Takwimu za kimataifa zinaonesha kuwa zaidi ya watu milioni 850 duniani wanaishi na aina fulani ya ugonjwa wa figo, huku takribani asilimia 10 ya watu wazima duniani wakiwa na dalili za ugonjwa huo. Aidha, mamilioni ya watu hulazimika kutegemea matibabu ya gharama kubwa kama dialysis au upandikizaji wa figo (kidney transplant) ili kuendelea kuishi.

Barani Afrika, tafiti zinaonesha kuwa kati ya asilimia 13 hadi 15 ya watu wazima wanaweza kuwa na dalili za ugonjwa wa figo. Nchini Tanzania, tafiti mbalimbali zinaonesha kuwa takribani asilimia 10 hadi 12 ya watu wazima wanaweza kuwa katika hatari au tayari wana dalili za ugonjwa wa figo, huku wengi wakigundulika katika hatua za mwisho za ugonjwa.

Gharama za matibabu ya magonjwa ya figo ni kubwa sana. Mgonjwa anayehitaji dialysis hulazimika kufanya matibabu hayo mara mbili hadi tatu kwa wiki, ambapo gharama ya kikao kimoja inaweza kufikia wastani wa dola za Marekani 80 hadi 200. Hii ina maana kuwa kwa mwaka mmoja, gharama za matibabu zinaweza kufikia dola 10,000 hadi 25,000 au zaidi kwa mgonjwa mmoja.

Aidha, matibabu ya upandikizaji wa figo (kidney transplant) yanaweza kugharimu kati ya dola 15,000 hadi 30,000, bila kujumuisha gharama za dawa za kudhibiti kinga ya mwili ambazo mgonjwa hulazimika kutumia maisha yote.

Kutokana na hali hii, ni wazi kuwa kinga ni bora zaidi kuliko tiba, na jamii inapaswa kuhamasishwa kuchukua hatua za kulinda afya ya figo mapema.

Katika muktadha huu, tiba asilia ina nafasi muhimu katika kusaidia kuimarisha kinga ya mwili na afya kwa ujumla. Hata hivyo, bado kuna changamoto ya uhaba wa ushahidi wa kisayansi unaothibitisha kwa kina baadhi ya dawa na mbinu za tiba asilia. Kwa sababu hiyo, TRAMEPRO inaendelea kusisitiza umuhimu wa tafiti za kisayansi, uthibitishaji wa dawa za asili, na ushirikiano kati ya wataalamu wa afya na taasisi za utafiti.

Kwa sasa, nikiwa katika ziara ya kitaaluma mjini New Delhi, India, ninapata uzoefu na kujifunza kuhusu matibabu mtambuka (Integrative Medicine) katika taasisi mbalimbali ikiwemo Max Super Speciality Hospital pamoja na taasisi za tiba asilia chini ya mfumo wa AYUSH. Uzoefu huu unalenga kuimarisha uelewa na ushirikiano katika kuunganisha tiba asilia na tiba za kisasa kwa manufaa ya afya ya jamii.

TRAMEPRO itaendelea kushirikiana na taasisi za utafiti, hospitali, na wataalamu wa magonjwa ya figo ili kuendeleza tafiti, kutoa elimu kwa jamii, na kuhakikisha matumizi salama na yenye tija ya tiba asilia.

Katika maadhimisho haya, ninatoa wito kwa:

Watabibu wa tiba asilia kuzingatia viwango vya usalama, maadili ya kitaaluma na uthibitisho wa kisayansi katika huduma wanazotoa.

Wananchi kuchukua hatua za kinga dhidi ya magonjwa ya figo ikiwa ni pamoja na kudhibiti shinikizo la damu na kisukari, kunywa maji ya kutosha, kutumia dawa kwa usahihi, na kufanya uchunguzi wa afya mara kwa mara.

Serikali na taasisi za utafiti kuendelea kuwekeza katika tafiti za dawa za asili na kuimarisha mfumo wa huduma za afya jumuishi.

Kwa pamoja tunaweza kujenga mfumo wa afya unaounganisha hekima ya tiba asilia na sayansi ya tiba ya kisasa kwa manufaa ya binadamu na mazingira yetu.

Mungu aibariki Tanzania na awajalie wananchi wake afya njema.

Boniventura Mwalongo Katibu Mkuu – TRAMEPRONew Delhi, India 12 Machi 2026



Ofisi ya BAKWATA Mkoa wa Singida, kupitia Sheikh wa Mkoa huo Issa Bin Nassoro, imezipongeza taasisi za Ramadhan Charity Programme2026, inayoongozwa na Ndugu Ahmed Misanga pamoja na Taasisi ya JAI Tanzania kwa kutoa sadaka katika Gereza la Manispaa ya Singida, misikiti pamoja na vituo vya watoto yatima.


Sheikh Issa amesema hayo leo wakati wa ziara yake ya kutembelea wafungwa katika Gereza la Manispaa ya Singida, ambapo pia walitoa sadaka ya Iftar kwa wafungwa ili waweze kupata futari pamoja na daku katika kipindi hiki cha mwezi mtukufu wa Ramadhani. Sadaka hizo zimetolewa na taasisi za Ramadhan Charity Programme 2026 pamoja na JAI Tanzania.

Katika hotuba yake, Sheikh Issa aliwaomba watu mbalimbali katika jamii kuwajali watu wenye mahitaji na masikini, akisisitiza kuwa kufanya hivyo ni jambo linalompendeza Mungu. Aliongeza kuwa hata mitume waliwahudumia na kuwasaidia watu masikini na wenye uhitaji.

Aidha, Sheikh wa Mkoa alitoa salamu kutoka kwa Mufti na Sheikh Mkuu wa Tanzania, Dkt. Abubakar Zubeir bin Ally, akisisitiza umuhimu wa kuendelea kuwajali watu wenye mahitaji maalum, wakiwemo wafungwa na makundi mengine yenye uhitaji katika jamii.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Ramadhan Charity Programme 2026, Ndugu Ahmed Misanga, amesema kuwa utoaji wa sadaka ya Iftar kwa watu wenye mahitaji ni utaratibu wao wa kila mwaka, hususan katika magereza na makundi mengine ya jamii. Amesema kuwa wamekuwa wakifanya shughuli hiyo kwa zaidi ya miaka mitano sasa.

Misanga alisisitiza kuwa watu waliopo magerezani wanahitaji huruma na faraja kutoka kwa jamii ili kuwapa moyo na kuwasaidia kumkaribia Mungu, ili wanaporudi uraiani wawe watu wema wenye hofu ya Mungu na mchango chanya kwa jamii.

Katika msaada huo, Ramadhan Charity Programme 2026 kwa kushirikiana na JAI Tanzania walitoa sadaka ya Iftar iliyojumuisha boksi la tende, sukari, tambi, mchele, ngano, juisi pamoja na taulo za kike kwa ajili ya wafungwa wanawake katika gereza hilo.

Naye Kaimu Mkuu wa Gereza la Wilaya ya Singida, Ndugu Amini Mjenza, amesema amefurahishwa na taasisi ya Ramadhan Charity chini ya uongozi wa Ahmed Misanga kwa kuwapatia sadaka ya Iftar, akieleza kuwa msaada huo utawasaidia sana wafungwa waliopo gerezani.

“Tutaitumia sadaka hii ya Iftar kama mlivyokusudia, na tunamuomba Mungu awalipie pale mlipotoa kwa ajili ya wafungwa wote, wanawake na wanaume,” amesema.
Katika tukio hilo, washiriki pia walipata nafasi ya kuliombea Taifa pamoja na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Taasisi ya Ramadhan Charity Programme 2026 imewataka Watanzania kutumia mwezi huu mtukufu wa Ramadhani kuwa wamoja, kusaidiana na kufanya kazi kwa pamoja katika kuwasaidia wenye mahitaji katika jamii.



 

Wakala wa Maendeleo ya Uongozi wa Elimu (ADEM) leo imepokea ujumbe wa wadau wa maendeleo kutoka taasisi mbalimbali ikiwemo Mastercard Foundation, Education for Sub-Saharan Africa (ESSA), Tanzania Education Network (TEN/MET), African Centre for School Leadership (ACSL), Teach United na Educate kwa ajili ya kujadili ushirikiano wa kuimarisha uongozi wa shule za sekondari nchini.

Akifungua kikao hicho, Mtendaji Mkuu wa ADEM, Dkt. Maulid J. Maulid, alieleza kuwa taasisi hiyo ina dhamana ya kitaifa ya kuwa kitovu cha ubora katika mafunzo, utafiti na ushauri kuhusu uongozi, usimamizi, utawala wa elimu pamoja na uhakiki wa ubora wa elimu.

Alisema kwa miongo kadhaa ADEM imekuwa mkono wa kimkakati wa Serikali katika kujenga uwezo wa wasimamizi wa elimu kuanzia wakuu wa shule, waratibu wa elimu wa kata, hadi maafisa wa elimu wa wilaya, mikoa na ngazi ya taifa.

“ADEM haijikiti tu kwenye mafunzo bali pia inafanya tafiti za kitaaluma zinazosaidia kuunda sera za elimu, kutoa huduma za ushauri kwa shule na halmashauri pamoja na kuandaa mifumo na zana za kuboresha utendaji wa shule. Kupitia mtandao mpana wa taasisi na maafisa wa elimu katika Mamlaka zote za Serikali za Mitaa, ADEM ina uwezo wa kutekeleza programu kubwa za kuimarisha uongozi na usimamizi wa shule nchini,” alisema Dkt. Maulid.

Katika kikao hicho, ADEM iliwasilisha maeneo yake muhimu ya utaalamu ikiwemo uongozi na utawala wa elimu, upangaji wa sera na uhakiki wa ubora, mipango ya maboresho ya shule, ufundishaji unaozingatia usawa wa kijinsia, uongozi wa kitaaluma wa ufundishaji, maendeleo ya taaluma ya walimu, ushirikishwaji wa jamii katika usimamizi wa shule pamoja na ufuatiliaji na tathmini ya mipango ya kimkakati ya shule.

Majadiliano pia yalijikita katika utekelezaji wa programu ya LIT-LEAD, inayotekelezwa kwa ushirikiano kati ya ADEM na VVOB – Education for Development kwa ufadhili wa Mastercard Foundation.

Programu hiyo inalenga kuziba pengo la uongozi katika shule za sekondari nchini kwa kuwajengea uwezo wakuu wa shule katika kuboresha ufundishaji na ujifunzaji, kukuza uongozi jumuishi unaozingatia usawa wa kijinsia, kuimarisha mipango ya maboresho ya shule pamoja na kuboresha utawala wa shule kupitia ushiriki wa kamati za shule na wazazi.

Kabla ya kuanza kwa utekelezaji wa programu hiyo, ADEM na VVOB zilifanya tathmini ya mahitaji ya mafunzo (Training Needs Assessment - TNA) iliyowahusisha viongozi wa shule, maafisa wa elimu wa wilaya pamoja na wawakilishi wa Wizara ili kuhakikisha maudhui ya mafunzo yanaendana na mazingira halisi ya elimu nchini Tanzania.

Akizungumza katika kikao hicho, Mkurugenzi wa VVOB nchini Tanzania, Bi. Sarish Hiribae, alipongeza ushirikiano uliopo kati ya VVOB na ADEM katika kuimarisha uongozi wa shule za sekondari nchini.

Kwa upande wake, kiongozi wa ujumbe wa wadau kutoka Mastercard Foundation, Bi. Tracy Osio, aliipongeza ADEM kwa ushirikiano wake na VVOB pamoja na wadau wengine, akieleza kuwa ushirikiano huo una uwezo mkubwa wa kuleta mageuzi katika uongozi wa elimu kupitia utekelezaji wa programu ya LIT-LEAD.

Katika majadiliano hayo, wadau pia waliuliza maswali kuhusu mifumo ya ADEM ya kuhakikisha ubora wa mafunzo yanayotolewa. Kujibu hilo, ADEM ilieleza kuwa ubora wa mafunzo huhakikishwa kupitia tathmini za mahitaji ya mafunzo, warsha za uthibitishaji wa maudhui pamoja na uhakiki wa ubora unaofanywa na Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (NACTVET) kwa kozi za muda mrefu.

Aidha, Dkt. Lucas Mzelela alieleza kuwa ushirikiano kati ya ADEM na VVOB ulianza mwaka 2025 na unatarajiwa kudumu kwa kipindi cha miaka sita. Katika kipindi hicho, taasisi hizo zitashirikiana kujenga uwezo wa wakuu wa shule za sekondari katika uongozi bora na usimamizi madhubuti wa elimu.

Aliongeza kuwa ushirikiano huo pia utahusisha uandaaji wa moduli za mafunzo kupitia mfumo wa kidijitali wa Learning Management System (LMS) ili kuwafikia viongozi wengi zaidi wa elimu nchini.

Kupitia ushirikiano wa kimkakati kama programu ya LIT-LEAD, ADEM inaendelea kuwa mhimili muhimu katika kuendeleza ajenda ya taifa ya kuboresha elimu na kuimarisha uongozi wa shule kwa manufaa ya wanafunzi nchini.










Wakala wa Maendeleo ya Uongozi wa Elimu - ADEM umeendesha mafunzo maalumu ya siku tano kwa Maafisa Elimu wa Mikoa 26 kutoka Tanzania Bara kuanzia tarehe 8-12 Machi, 2026 jijini Arusha.

Mafunzo hayo yalilenga kuwajengea uwezo viongozi hao wa kuimarisha uongozi na usimamizi wa sekta ya elimu katika maeneo mbalimbali ikiwemo uandaaji wa Mpango Mkakati wa elimu katika ngazi ya mkoa, utafutaji na usimamizi wa rasilimali katika elimu, utambuzi na usimamizi wa changamoto za afya ya akili kwa watumishi wa kada ya elimu, mbinu bora za kushughulikia malalamiko, kufanya ufunzaji na uatamizi, na kuimarisha usimamizi saidizi katika sekta ya elimu.

Akifunga mafunzo hayo, Kamishna wa Elimu nchini, Dkt. Lyabwene M. Mtahabwa, amesisitiza umuhimu kwa viongozi wote wa elimu kuanzia ngazi ya kitaifa hadi shule kuweka mbele haki za watoto katika utekelezaji wa majukumu yao.

Amesema kuwa watoto ndio msingi wa uwepo wa nafasi za uongozi katika sekta ya elimu, hivyo viongozi wanapaswa kuhakikisha wanawalinda na kuwapatia mazingira bora ya kujifunzia.

Aidha, Dkt. Mtahabwa amewataka Maafisa Elimu wa Mikoa kuacha mtindo wa uongozi unaolenga kutafuta makosa kwa nia ya kuwaadhibu wanaowaongoza na badala yake, amewahimiza kutumia mbinu za kutoa msaada wa kitaaluma na kitaalamu kwa watumishi wa elimu, kama walivyojifunza wakati wa mafunzo hayo.

“Ni muhimu viongozi wa elimu kuwa washauri na wawezeshaji kwa wale wanaowaongoza, badala ya kuwa wakaguzi wanaotafuta makosa,” Amesisitiza Dkt. Mutahabwa

Kamishna wa elimu pia, amesisitiza kuwa Serikali pamoja na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kupitia taasisi zake ikiwemo ADEM, imejipanga kuhakikisha mtoto wa Kitanzania anapata elimu bora katika mazingira salama.

Amesema ili kufikia lengo hilo, kila kiongozi wa elimu anapaswa kusimamia kikamilifu majukumu yake katika eneo analoliongoza.

Mafunzo hayo ni sehemu ya jitihada za Serikali kuendelea kuimarisha uwezo wa viongozi wa elimu ili kuboresha utoaji wa elimu nchini.

Jumla ya Maafisa Elimu wa Mikoa 26 kutoka katika Mikoa yote ya Tanzania Bara wameshiriki mafunzo hayo yaliyoendeshwa na ADEM kwa ufadhili wa mradi wa Shule Bora.












Na Mwandishi wetu, Tabora

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imeridhishwa na Ujenzi wa Kiwanda cha Zege kinachomilikiwa na kampuni tanzu ya TANESCO ya  kuzalisha nguzo za zege  kilichopo katika Mkoa wa Tabora wakati wa ziara yao ya kikazi Mkoani humo tarehe 12 Machi, 2026.

Akizungumza baada ya ziara hiyo Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Subira Mgallu ameeleza kuridhishwa na   hatua ya kukamilika kwa Kiwanda hicho kilichoanza uzalishaji  na kuwaelekeza Wizara ya Nishati  na TANESCO kukisimamia kiwanda hiko kiendelee kufanya kazi kwa ufanisi mkubwa na kuzalisha faida.

"Kwa niaba ya Kamati tumeridhika na kazi kubwa iliyofanyika katika kiwanda hiki ambacho kimekamilika na uzalishaji umeanza, tunatoa rai kwa Wizara na TANESCO kuendelea kusimamia kiwanda hiki ili kiendelee kufanya kazi yake kwa ufanisi zaidi", alieleza Mhe. Mgallu

Alieleza kuwa uelekeo wa sasa ni kusambaza nguzo za zege hasa kwa maeneo yenye unyevu sambamba na maeneo yaliyo karibu na misitu pamoja na mikondo ya mito ya maji ambayo nguzo za miti huathirika kwa kiasi kikubwa haswa kwenye msimu wa mvua hivyo nguzo za zege zitakuwa msaada mkubwa katika mazingira kama hayo na  kuboresha upatikanaji wa huduma ya umeme.

“Kama mnavyofayahamu kwa sasa uelekeo ni kusambaza nguzo za zege badala ya nguzo za miti hasa katika maeneo ambayo yana asili ya unyevu, maeneo karibu na mito ya maji ama visiwa ambapo nguzo za miti huathiriwa na mazingira hayo”, aliongeza. 

Naye Mhe. Deogratius Ndejembi Waziri wa Nishati alisema kuwa ujenzi wa kiwanda hiko umekamilika mwaka huu na kuanza uzalishaji wake rasmi Februari, 2026 ambapo mpaka sasa wastani wa nguzo zinazozalishwa ni 80 hadi 120 kwa siku ambapo mpaka sasa gharama ya shilingi bilioni 6.4 imeshatumika katika hatua zote hadi uzalishaji ulipoanza ambapo kiasi cha shilingi bilioni 1.4 bado hazijalipwa kwa mkandarasi ambaye bado yupo kwenye kipindi cha uangalizi.

“Kiwanda hiki kilianza uzalishaji rasmi mwezi Februari mwaka huu ambapo kwa sasa kina uwezo wa kuzalisha nguzo 80 hadi 120, mpaka sasa ujenzi wa kiwanda hiki hadi uzalishaji ulipoanza imetumia gharama ya shilingi bilioni 6.4 ambapo bado kuna billioni 1.6 bado haijalipwa kwa mkandarasi kwa kuwa yupo kwenye kipindi cha uangalizi”, aliongeza Mhe. Ndejembi. 

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO Bw. Lazaro Twange ameeleza kuwa kukamilika kwa kiwanda hiko kunaenda kuleta mageuzi makubwa kwani nguzo za zege ni teknolojia ambayo bado inakuwa hivyo Shirika bado linaendelea kuikuza sekta  na kuwa na utoshelevu wa nguzo zenyewe kwa matumizi ya wananchi. 

“Baada ya kukamilika kwa ujenzi wa kiwanda na kuanza uzalishaji ambapo kwa hali ilivyo ya matumizi ya nguzo za zege ni teknolojia ambayo bado inakuwa hivyo kama Shirika tutahakikisha tunaisimamia sekta hii ili kuendelea kuwapatia wateja wetu huduma ya umeme wa uhakika”, alisema Bw. Twange. 

Ziara hiyo ya kamati ya kudumu ya bunge ya nishati na madini inalenga kufanya ukaguzi wa miradi mbalimbali inayotekelezwa na Shirika katika maeneo mbalimbali nchini ili kujionea ufanisi wake.





 


Top News