Na Elimu ya Afya kwa Umma
SERIKALI kupitia Wizara ya Afya imewahimiza Watanzania kurejea katika matumizi ya vyakula vya asili kama sehemu muhimu ya kujenga afya bora, kuzuia magonjwa, na kusaidia matibabu kwa njia salama na endelevu.

Akizungumza jijini Dodoma katika Mkutano wa Waziri wa Afya na wataalam wa tiba asili, Mkurugenzi wa Huduma za Uhamasishaji wa Afya (Elimu ya Afya kwa Umma), Dkt. Rahma Ahmed Hingora, amesema vyakula vya asili vina mchango mkubwa katika kuimarisha afya ya mwili na vinaweza kutumika kama sehemu ya kinga na tiba iwapo vitatumika kwa usahihi.

“Tunapaswa kurudisha utamaduni wa kula vyakula vya asili kama maboga, ubuyu na vyakula vingine vinavyopatikana katika mazingira yetu. Hivi ni vyakula vyenye virutubishi muhimu vinavyosaidia kuimarisha kinga ya mwili na afya kwa ujumla,” amesema Dkt. Hingora.

Amebainisha kuwa kumekuwa na mabadiliko ya mtindo wa maisha ambapo jamii imekuwa ikipuuza vyakula vya asili na kuelekea zaidi katika matumizi ya vyakula vilivyosindikwa, ambavyo mara nyingi hupoteza virutubisho muhimu na vinaweza kuongeza hatari ya magonjwa yasiyoambukiza.

“Ni muhimu kuepuka matumizi yasiyo ya lazima ya kemikali na virutubisho bandia kwenye vyakula. Turejee kula vyakula katika hali yake ya asili. Kula chakula kama dawa, na usisubiri kula dawa kama chakula,” amesisitiza.

Aidha, Dkt. Hingora amesema Serikali itaendelea kuimarisha utoaji wa elimu ya afya kwa wananchi kupitia vyombo mbalimbali vya habari, majukwaa ya kidijitali, pamoja na Wahudumu wa Afya Ngazi ya Jamii, ili kuhakikisha jamii inapata uelewa sahihi kuhusu lishe bora na matumizi salama ya vyakula vya asili.

Katika mkutano huo, Waziri wa Afya, Mhe. Mohamed Mchengerwa, alisisitiza umuhimu wa kuunganisha maarifa ya tiba asili na tiba ya kisasa, huku akihimiza wataalam kuongeza juhudi za kutoa elimu kwa jamii kuhusu mchango wa vyakula vya asili katika afya.

Serikali inaamini kuwa matumizi sahihi ya vyakula vya asili yanaweza kusaidia kupunguza hatari ya magonjwa, kuimarisha kinga ya mwili, na kuchangia ustawi wa afya ya wananchi kwa ujumla.

 
Waziri wa Fedha wa Tanzania, Khamis Mussa Omar umza wakati wa mkutano huo uliofanyika leo Machi 26, 2026 jijini Dar es Salaam wakati kujadiliana juu ya uwekezaji na biashara yenye thamani ya dola za Marekani bilioni 7.8 nchini Tanzania katika mkutano wa Bodi ya taasisi hiyo.



Na Mwandishi Wetu

AFRICAN Trade & Investment Development Insurance (ATIDI) imejadili uwekezaji na biashara yenye thamani ya dola za Marekani bilioni 7.8 nchini Tanzania katika mkutano wa Bodi ya taasisi hiyo uliofanyika jijini Dar es Salaam, hatua inayolenga kuimarisha mazingira ya biashara na kuvutia uwekezaji wenye mitaji mikubwa.

Akizungumza wakati wa mkutano huo uliofanyika leo Machi 26, 2026 jijini Dar es Salaam, Waziri wa Fedha wa Tanzania, Khamis Mussa Omar amesema kufungua uwezo kamili wa uchumi wa Tanzania kunahitaji ushirikiano imara unaoweza kuhamasisha mitaji mikubwa ya uwekezaji.

Amesema ATIDI imekuwa mshirika muhimu katika kupunguza hatari za uwekezaji, hali inayosaidia kuvutia mitaji ya sekta binafsi na kuwezesha utekelezaji wa miradi mikubwa ya maendeleo.

Pembeni mwa mkutano huo, uongozi wa ATIDI ulikutana na maafisa wa serikali, taasisi za kifedha, washirika wa maendeleo pamoja na wadau wa sekta binafsi kujadili namna ya kuimarisha zaidi mazingira ya biashara na uwekezaji nchini.

Majadiliano hayo yaliambatana na warsha ya wadau wa ngazi ya juu iliyopewa jina la “Kuimarisha Mazingira ya Biashara na Uwekezaji Tanzania,” iliyolenga kuboresha mfumo wa kifedha na kuongeza upatikanaji wa mitaji kwa ajili ya miradi ya maendeleo.

Washiriki wa mkutano huo walisisitiza umuhimu wa kupata suluhisho la pamoja katika kuongeza mtiririko wa mitaji kutoka sekta binafsi ili kuwezesha upatikanaji wa fedha kwa gharama nafuu katika sekta muhimu za uchumi na kukuza biashara za kikanda.

Tanzania ina nafasi ya kipekee katika historia ya ATIDI ikiwa ni miongoni mwa nchi wanachama waanzilishi tangu kuanzishwa kwa taasisi hiyo mwaka 2001 kwa msaada wa Common Market for Eastern and Southern Africa (COMESA) na World Bank.

Kwa mujibu wa takwimu za taasisi hiyo, kwa kipindi cha miaka 25 iliyopita ATIDI imewezesha uwekezaji na biashara za mipakani barani Afrika zenye thamani ya zaidi ya dola za Marekani bilioni 93 kupitia huduma zake za bima ya mikopo ya biashara na uwekezaji.

Nchini Tanzania pekee, taasisi hiyo imesaidia zaidi ya sera 200 za bima, hatua iliyowezesha biashara na uwekezaji wenye thamani ya dola bilioni 7.8 huku kiwango cha hatari kinachodhibitiwa kikiwa karibu dola bilioni 1.8.

Uwekezaji huo umeelekezwa katika sekta muhimu za maendeleo ikiwemo miundombinu, nishati, mawasiliano na makazi nafuu.

Miongoni mwa miradi mikubwa iliyoungwa mkono ni reli ya kisasa ya Standard Gauge Railway (SGR) Tanzania ambayo imeendelea kuimarisha nafasi ya Tanzania kama kitovu cha biashara na usafirishaji katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa ATIDI, Manuel Moses amesema changamoto kubwa kwa Afrika si ukosefu wa fursa bali ni hatari zinazohusiana na uwekezaji.

Naye Mtaalamu Mkazi wa Bima wa ATIDI, Tusekile Kibonde amesema taasisi hiyo inaendelea kutoa suluhisho za kupunguza hatari zinazowezesha upatikanaji wa fedha kwa miradi mikubwa barani Afrika huku akibainisha kuwa ushirikiano huo unasaidia kubadilisha fursa za uwekezaji kuwa ukuaji endelevu wa uchumi.






MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Tanzania Bara Stephen Wasira amesema Chama kinapata maendeleo kutokana na ukubwa wake, kusimamia, ahadi na imani kubwa ya wananchi kwa Chama.

Kauli ya Wasira imekuja siku chache baada ya Kiongozi kutoka katika chama kimoja Cha Upinzani na kudai CCM inabebwa na serikali.

Wasira meyasema hayo leo Machi 26, 2026 alipozungumza baada ya kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa jengo la ofisi za Chama Mkoa wa Geita ambalo ujenzi wake unatarajiwa kutumia sh bilioni 1.5.

“Tulipokuwa tunakuja mtu mmoja akanipa simu yake nimsikilize mkubwa mmoja wala sitaki kumtaja jina, anadai CCM ni Chama kinabebwa na serikali, sasa ningemwalika hapa aone tumejenga hapa atwambie kasma namba ngapi imeleta pesa Geta.

“Unajua ukikosa la kusema na mdomo unao unaweza kusema chochote kwani usiposema chochote mdomo utakosa kazi utakuwa unakula tu bila kusema na mdomo una kazi ya kula na kusema.








WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amewaomba Watanzania waendelee kumuombea kwa Mwenyezi Mungu aliyekuwa Waziri Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, marehemu William Lukuvi aliyefariki jana Machi 25, 2026 katika Hospitali ya Benjamin Mkapa, jijini Dodoma.

Akiongea kwa niaba ya Serikali nyumbani kwa marehemu Area D, jijini Dodoma leo, Alhamisi, Machi 26, 2026, Waziri Mkuu amesema: “Kwa niaba ya Serikali natoa pole kwa familia, ndugu, jamaa. Jambo hili zito, gumu kulielewa, gumu kulipokea.”

…Lakini ndio limeshatufika na sote hatukutarajia maana Mheshimiwa Waziri alikuwa kazini. Tuendelee kumuombea kwa Mwenyezi Mungu na kuifariji familia. Mwenyezi Mungu awaimarishe kwa sababu yeyé ndio mfariji mkuu,” amesisitiza.

Vilevile, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu ametumia fursa hiyo kuihakikishia familia kwamba Serikali itaendelea kuwa pamoja nayo katika kipindi hiki chote cha majonzi.

 Viongozi wengine waliokuwepo msibani hapo ni pamoja na Naibu Spika, Daniel Siro, Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais, (Muungano na Mazingira), Mhandisi Hamad Masauni, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumisi wa Umma na Utawala Bora), Ridhiwani Kikwete, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule na Katibu Tawala wa Mkoa wa Arusha, Dkt. Toba Nguvila.













Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye pia ni Makamu wa Pili wa Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika (AU), akishiriki Kikao cha Baraza la Uongozi la Umoja wa Afrika (African Union Bureau of Assembly) kilichofanyika kwa njia ya mtandao, tarehe 26 Machi, 2026, Ikulu Ndogo ya Tunguu, Zanzibar. 

Kikao hicho kiliongozwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika (AU) Rais wa Jamhuri ya Burundi Mhe. Évariste Ndayishimiye.






 Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, leo tarehe 26 Machi 2026 amewasili Jijini Malabo nchini Guinea ya Ikweta, ambapo anamwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Jumuiya ya Nchi za Afrika, Karibiani na Pasifiki, utakaofanyika kuanzia tarehe 27 hadi 29 Machi 2026.

Katika Mkutano huo, Tanzania itapata fursa ya kuwasilisha vipaumbele vyake vya Kitaifa pamoja na kuchangia kuunda mwelekeo wa mikakati mipya ya jumuiya hiyo, inayoelekea kutimiza miaka 50 tangu kuanzishwa kwake.

Ushiriki wa Tanzania katika Mkutano huo ni mwendelezo wa jitihada za kuendelea kushiriki kikamilifu katika majukwaa ya kikanda na kimataifa, na kudhihirisha mchango wa nchi katika mijadala ya maendeleo na ushirikiano wa kimataifa.

Aidha, Makamu wa Rais anatarajiwa kufanya mazungumzo ya pande mbili na viongozi mbalimbali wanaoshiriki Mkutano huo kwa lengo la kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi na kimaendeleo.












• TBL na viongozi wa jiji waungana kulinda mifumo ya maji taka Dar es Salaam

• Kampeni ya usafi inaonyesha utekelezaji wa vitendo wa ahadi za uendelevu na uwajibikaji kwa jamii

• Ushirikiano unaonesha athari halisi ya kimazingira pale biashara inaposhirikiana na jamii.

Tanzania Breweries PLC (TBL PLC) imeadhimisha Siku ya Maji Duniani kwa kuchukua hatua za moja kwa moja, ikiwaleta pamoja viongozi wa jiji, wafanyakazi zaidi ya 100, na wadau wa jamii katika zoezi la usafi katika Wilaya ya Ilala.

Mpango huo ulilenga kurejesha mfereji wa kutolea maji machafu, eneo lenye mchango mkubwa katika kulinda mifumo ya maji inayozunguka. Zoezi hilo lilifanyika kwa ushirikiano na Meya wa Jiji la Dar es Salaam, Nurdin Bilal Juma, pamoja na uongozi wa Manispaa ya Ilala na madiwani wa maeneo husika, likionyesha dhamira ya pamoja ya kulinda usalama wa maji mijini na afya ya umma.

Likiongozwa na Neema Temba, Mkurugenzi wa Masuala ya Kampuni wa Tanzania Breweries Limited, zoezi hilo liliwakutanisha wafanyakazi na mamlaka za mitaa kushughulikia hitaji halisi la kimazingira kupitia vitendo vya moja kwa moja. Kampuni ilisaidia mpango huo kwa kutoa vifaa na rasilimali, hivyo kuwawezesha washiriki kuhakikisha maboresho yanayopimika katika usafi na kulinda miundombinu ya maji ya pamoja.

Akizungumza wakati wa zoezi hilo, Neema Temba alisema mbinu ya kampuni katika usimamizi wa maji inajikita katika vitendo na uwajibikaji wa muda mrefu. “Maji yako katikati ya biashara yetu na jamii zetu. Tuna wajibu wa kuyahifadhi, ndani ya shughuli zetu na katika mazingira tunayofanyia kazi. Mpango huu unaonyesha jinsi tunavyoshirikiana na wadau kutoa suluhisho za vitendo zinazosaidia usalama wa maji kwa muda mrefu.”

Alisisitiza pia umuhimu wa kuunganisha hatua za ngazi ya jamii na vipaumbele vya kimazingira kwa ujumla. “Usimamizi wa maji unahitaji juhudi endelevu katika shughuli za kampuni na jamii. Shughuli kama hizi huongeza uelewa na kuonyesha kuwa athari halisi hutokana na ushirikiano na hatua za moja kwa moja.”

Mbali na mpango huu wa eneo husika, Tanzania Breweries PLC inaendelea kuwekeza katika juhudi za muda mrefu za uhifadhi wa maji kupitia ushirikiano unaolenga kuboresha upatikanaji wa maji na kulinda mifumo ya ikolojia.

Nurdin Bilal Juma, Meya wa Jiji la Dar es Salaam, alibainisha kuwa ushirikiano kati ya sekta binafsi na serikali za mitaa ni muhimu katika kudumisha viwango vya mazingira mijini. “Kudumisha usafi wa jiji letu na kulinda mifumo ya maji ni jukumu la pamoja. Ushirikiano kama huu unaunga mkono jitihada zetu za kuboresha usafi wa mazingira, kulinda afya ya umma, na kujenga jiji endelevu kwa wakazi wote.”

Kwa kushirikiana na WWF Tanzania, kampuni imeunga mkono miradi ya kuboresha usalama wa maji katika maeneo kama Kibaha, ikiwemo uwekaji wa miundombinu ya maji inayotumia nishati ya jua ambayo hutoa maji safi na ya kuaminika kwa jamii zinazozunguka. Mipango hii pia inahamasisha matumizi endelevu ya maji na ulinzi wa mazingira kupitia suluhisho zinazotegemea asili zinazosaidia kuimarisha mifumo ya ikolojia na maeneo ya vyanzo vya maji.

TBL na WWF pia wanafanya kazi pamoja katika juhudi pana za usalama wa maji jijini Dar es Salaam, wakizingatia ulinzi na urejeshaji wa vyanzo muhimu vya maji kama vile mifumo ya mito ya Msimbazi, Kizinga, na Ruvu, ambayo ni muhimu kwa upatikanaji wa maji wa muda mrefu wa jiji.

Ingawa zoezi la usafi ni la eneo maalum, linaakisi dhamira pana ya usimamizi bora wa maji na linaonesha umuhimu wa ushirikiano katika kukabiliana na changamoto za kimazingira kupitia suluhisho za vitendo.











Top News