Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na Rais wa Jamhuri ya Singapore, Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam mara baada ya kuwasili Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa Ziara ya Kitaifa, tarehe 09 Juni, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Singapore, Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam, ambaye amewasili nchini kwa ziara ya Kitaifa ya siku 3, kufuatia mwaliko wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na mwenyeji wake mara baada ya kuwasili ikulu.

Mheshimiwa Rais Tharman Shanmugaratnam ameweka historia ya kuwa Rais wa kwanza kutembelea nchini tangu kuanzishwa kwa mahusiano ya kidiplomasia mwaka 1980.







Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kuiimarisha mifumo ya usimamizi wa nyaraka za kieletroniki ili kuhakikisha taarifa muhimu za Taifa zinahifadhiwa kwa usalama, zinapatikana kwa urahisi na zinadumu kwa muda mrefu.

Hayo yamemwa na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abulla katika maadhimisho ya siku ya nyaraka duniani kwa mwaka 2026 yaliyoadhimisha kitaifa katika viwanja vya Makumbusho ya Amani Mnazi mmoja.

Amesema katika kipindi hiki cha maendeleo makubwa ya teknolojia ya habari na mawasiliano usimamizi wa nyaraka unahitaji kwenda sambamba na matumizi ya mifumo ya kisasa ya kidijitali ili kurahisha upatikanaji wa taarifa na kuongeza ufanisi zaidi.

Mhe Hemed amesema kuwa ni matumaini ya Serikali kuwa taasisi zote za umma na binafsi zitaendelea kuzingatia viwango vya kitaalamu katika usimamizi wa nyaraka na kumbukumbu kwa lengo la kuongeza ufanisi wa utoaji huduma kwa wananchi na kulinda historia ya Taifa la Tanzania.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar amesema kuwa Zanzibar imekuwa kitovu muhimu cha elimu, biashara, ustaarabu na utamaduni katika ukanda wa Afrika Mashariki na bahari ya hindi hivyo Serikali itahakikisha kuwa Manuskripti zinaendelea kuhifadhi maarifa muhimu yanayohusu dini, sheria, elimu, tiba , biashara, utawala na maisha ya jamii kwa ujumla.

Aidha amesema kuwa hati za kale ni ushahidi tosha wa mchango mkubwa wa Zanzibar katika maendeleo ya elimu na ustaarabu wa kiislamu sambamba na kuwa chanzo muhimu cha tafiti kwa watafiti , wanahistoria, wanafunzi na taasisi mbali mbali duniani.

Sambamba na hilo Mhe. Hemed amesema ni wajibu wa kila mmoja kuhakikisha kuwa manuskripti na nyaraka adhimu zinalindwa, zinatunzwa na zinaendelezwa kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho na kuahidi kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na taasisi mbali mbali za ndani na nje ya nchi katika kuhifadhi na kuendeleza urithi huu muhimu kwa Taifa.

Hata hivyo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar ametoa wito kwa wananchi kuthamini utamaduni wa kutunza kumbukumbu na nyaraka muhimu katika maisha yao binafsi, taasisi na jamii kwa ujumla kwani Taifa lenye utamaduni wa kuhifadhi kumbukumbu zake hujenga msingi imara wa maendeleo, uwajibikaji na utambulisho wa vizazi vyake.

Nae waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Ikulu Mhe. Dkt. SAADA MKUYA SALUM amesema uwepo wa taasisi ya Nyaraka huisaidia jamii kujua umuhimu wa nyaraka na kumbukumbu katika kuhifadhi historia, kulinda haki za wananchi, kuimarisha uwazi na uwajibikaji pamoja na kuchangia maendeleo endelevu katika jamii.

Amesema nyaraka ni msingi wa kumbukumbu za Taifa zinazohifadhi ushahidi wa shughuli za Serikali na jamii pamoja na kulinda haki za wananchi, kuimarisha utawala bora na kutoa rejea muhimu kwa vizazi vya sasa na vijavyo.

Aidha Dkt. Saada amefahamisha kuwa katika kuadhimisha siku ya nyaraka duniani taasisi ya nyaraka na kumbukumbu Zanzibar imeandaa na kutekeleza shughili mbali mbali ikiwewmo jukwaa la nyaraka, ziara za kijamii, maonesho ya nyaraka za kihistoria sambamba na maonesho maalumu ya maandiko ya kiislamu na hati za kiarabu.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Nyaraka na kumbukumbu Zanzibar ndugu Khatibu Suleiman Khatibu amesema taasisi hio imejipanga kutoa elimu juu ya matumizi mazuri ya nyaraka na kumbukumbu kwa maslahi ya vizazi vya sasa na baadae.

Ndugu Khatibu ametumia nafasi hio kuitaka jamii kuitumia taasisi ya nyaraka katika utunzaji wa nyaraka na kumbukumbu pamoja na kupata elimu juu ya utunzaji wa nyaraka na kujiepusha na migogoro isiokuwa na tija katika jamii

Mapema Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar amekagua mabanda ya maonesho ya vitu vya asili na tamaduni za kizanzibari.









Na Mwandishi Wetu

KATIKA kuelekea kusherehekea siku ya kucheza duniani (International day of play), Shirika lisilo la kiserikali la BRAC Tanzania limewataka wazazi kutenga muda wao mzuri wa kucheza na watoto ili kuwapa ujasiri na kupata uchangamshi wa kimwili na kiakili.

Hayo yamesemwa na mkufunzi wa makuzi na malezi na maendeleo ya awali ya watoto (ECD Trainer) Mbua Dule wakati wa kuadhimisha siku hiyo ya kucheza duniani kwa kutambua umuhimu wa wazazi kushiriki kwenye michezo ya watoto.

Mbua amesema, jamii ya sasa hivi ni tofauti na jamii ya zamani ambapo wazazi wengi kwa sasa hawana muda wa kukaa na mtoto zaidi anaangalia harakati zake za kimaisha na kusahau majukumu yake kama mzazi au mlezi.

Amesema, mzazi anapocheza na mtoto kunakuwa na muunganiko mzuri wa mahusiano ya mzazi na mtoto, na uoga huwa unapungua na hata ikitokea mtoto amefanyiwa ukatili wa kijinsia wa aina yoyote ile basi anakuwa na uwezo wa kuelezea kwa mzazi wake au mlezi.

“wazazi wengi wamekuwa hawana muda wa kukaa na watoto, ukipata muda wa kucheza na mtoto wako basi unakuwa unampa ujasiri wakati wote na hata anapokwua changamoto ya kufanyiwa ukatili wa kijinsia basi anaweza akakufuata na kukuelezea jambo hilo sababu tayari anakuwa ameshajenga ukaribu Zaidi wa mtoto na mzazi,” amesema Dule.

Amesema, kila mwaka tarehe Juni 11, ni Siku ya kucheza duniani na wao kama BRAC wameamua kushiriki kwa vitendo,wakianzia kwenye maeneo ya jamii na kumalizia kwa wafanyakazi sababu hata pindi wanapliwa wanarudi nyumbani wafahamu umuhimu wa kutenga muda wa kucheza na mtoto.

“tumeanza kwenye jamii katika vituo mbalimbali vya malezi na makuzi ya awali kwa watoto lakini kwa siku ya leo tumeamua kuwashirikisha wafanyakazi , tuwaoe elimu juu ya umuhimu wa kutenga muda wa kucheza na mtoto na hata wanapokuwa wanarudi majumbani wawe wakawa mabalozi wa kuwaelimisha jamii umuhimu wa kutenga muda wa kucheza na watoto wao,”amesema Dule

Dule amesema, duniani ya sasa hivi imetawaliwa na utandawazi zipo katuni zinazotoa elimu, watoto wengi wamekuwa wanatumia muda mwingi kwenye simu za wazazi wao jambo ambalo linawanyima fursa ya kupata muda wa kucheza, hivyo basi wazazi au walezi watenge japo muda wa asilimia 20 hadi 30 kwa ajili ya watoto kucheza ili kukuza uchangamfu wa mwili na akili.

Shirika la BRAC limekuwa linatoa elimu ya makuzi na malezi ya awali kwa wanafunzi katika vituo mbalimbali na wamekuwa wanatoa elimu ya malezi kwa wazazi, ulinzia na usalama kwa watoto. Na vituo hivyo vimekuwa vinatoa fursa ya mabinti zaidi ya 300 kupata fursa ya ajira.
Wafanyakazi wa Shirika la Brac Tanzania wakicheza michezo mbalimbali wakati ya maadhimisho ya siku ya kucheza duniani iliyofanyika katika Makao Makuu ya Ofisi hiyo Jijini Dar es Salaam.





Na Mwandishi wetu, TBN, Dar es salaam

Balozi wa Uganda nchini Tanzania, Balozi Kanali Mstaafu Fred Mwesigye, ametangaza kuandaa kikao maalumu kitakachowakutanisha viongozi wa Baraza la Habari Afrika Mashariki chini ya uenyekiti wa David Omwoyo, Mtendaji Mkuu wa Baraza la Habari Kenya kujadili mikakati ya kuendeleza utalii wa kiutamaduni, uchumi wa ubunifu na sekta ya michezo inayokua kwa kasi katika ukanda huu.

Hatua hiyo inafuatia kikao cha ngazi ya juu kilichofanyika jijini Dar es Salaam kilichowakutanisha Balozi Mwesigye, Katibu Mtendaji wa Baraza la Habari Tanzania, Ernest Sungura, pamoja na wawakilishi wa Umoja Conservation Trust (UCT) wakiongozwa na Bryan Toshi , ambacho kilijadili kwa kina nafasi ya vyombo vya habari katika kujenga Shirikisho la Afrika Mashariki na kuharakisha umoja wa kikanda.

Katika kikao hicho, washiriki walikubaliana kwamba tasnia ya habari katika Afrika Mashariki inapaswa kuondokana na mtazamo wa kuripoti matukio ya kitaifa kwa namna ya kujitenga, na badala yake kujenga simulizi la kikanda linaloangazia matarajio, urithi na fursa za pamoja kwa wananchi wote.

Balozi Mwesigye alibainisha kuwa mjadala huu umejengwa juu ya maono ya kudumu ya waasisi wa Afrika Mashariki, hususan Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Mzee Jomo Kenyatta, ambayo yana umuhimu mkubwa leo kuliko wakati mwingine wowote katika historia kwani katika dunia inayozidi kutawaliwa na miungano mikubwa ya kikanda, Afrika Mashariki lazima iimarishe umoja wake ili kuongeza uimara wa kiuchumi, ushawishi wa kimkakati na ustawi wa pamoja.

Kauli hiyo pia inaenda sambamba na Hotuba ya Hali ya Taifa ya mwaka 2026 ya Rais wa Uganda, Yoweri Kaguta Museveni Tibuhaburwa, ambapo alithibitisha tena dhamira thabiti ya Uganda ya kuendeleza Shirikisho la Kisiasa la Afrika Mashariki na ushirikiano mpana wa Bara la Afrika akisisitiza kuwa ushirikiano wa kiuchumi na kisiasa ndiyo jibu sahihi kwa swali la ustawi wa kiuchumi na usalama wa muda mrefu.

Naye Ernest Sungura, ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa Baraza la Habari Afrika Mashariki na Katibu Mkuu wa Baraza la Habari Duniani, alieleza kuwa vyombo vya habari lazima viwe daraja linalowaunganisha wananchi badala ya kuwa mipaka inayowatenganisha, na kuongeza kuwa ushirikiano wa kikanda utafanikiwa pale wananchi watakapoanza kujiona kama Waafrika Mashariki kwa kawaida sawa na wanavyojiona kupitia mataifa yao kama Tanzania, Uganda, Kenya, Rwanda, Burundi, Sudan Kusini, Kongo au Somalia.

Kikao hicho kiliangazia changamoto ya muda mrefu inayolikabili eneo hili ikiwemo uwepo wa masoko yaliyogawanyika na mitazamo finyu ya kitaifa ambayo mara nyingi huzuia ukanda huu kufikia uwezo wake kamili, huku kikisisitiza kuwa Afrika Mashariki iliyounganishwa kikamilifu ingekuwa na nguvu kubwa zaidi ya majadiliano ya kiuchumi, soko pana, mvuto kwa wawekezaji na ushawishi mkubwa wa kisiasa duniani.

Moja ya maeneo makuu ya kimkakati yaliyojadiliwa ni maandalizi ya michuano ya kihistoria ya AFCON 2027 itakayoandaliwa kwa pamoja na mataifa ya Afrika Mashariki, ambapo Balozi Mwesigye alisisitiza kuwa mashindano hayo yanapaswa kutazamwa kama mradi wa mageuzi ya kikanda badala ya tukio la michezo pekee, kwani yanatoa jukwaa la kuonesha fursa za uwekezaji, vivutio vya utalii na uwezo wa kushirikiana kama ukanda mmoja.

Akichangia mada hiyo, Bryan Toshi wa Umoja Conservation Trust alieleza kuwa mafanikio ya kweli ya AFCON 2027 yatapimwa kwa yale yatakayotokea kabla, wakati na baada ya mashindano, huku akihimiza matumizi ya simulizi zenye uratibu ili kuzalisha ajira na kuimarisha mshikamano wa watu kwa watu.

Aidha, washiriki waligusia umuhimu wa Kiswahili kama nyenzo kuu ya kuunganisha tamaduni na diplomasia ya kikanda, ambapo walijadili uwezekano wa kushirikiana na Sekretarieti ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ili kuanzisha rasmi Wiki ya Kiswahili ya Jumuiya ya Afrika Mashariki inayopendekezwa kufanyika kila mwaka kuanzia tarehe 1 hadi 7 Julai.

Naye Ernest Sungura alikumbusha kuwa ushirikiano wa kikanda unahusu watu kwanza, na ingawa masuala ya miungano ya forodha na korido za biashara ni muhimu, ushirikiano wa kweli hufanikiwa pale watu wanapowasiliana na kuelewana kupitia maono ya pamoja yanayojengwa na vyombo vya habari.

Ujumbe mkuu uliotoka katika kikao hicho cha Dar es Salaam ulibaki kuwa wazi kwamba Shirikisho la Afrika Mashariki halitajengwa na serikali pekee, bali litajengwa kupitia mawazo, utamaduni, lugha, michezo na simulizi zinazowaunganisha wananchi, huku vyombo vya habari vikiwa injini kuu muhimu ya kuifikisha Afrika Mashariki kwenye hatima yake ya kuwa na nguvu na ustawi wa pamoja.


Na Janeth Raphael MichuziTv - Bungeni Dodoma

Serikali imeeleza kuwa inaendelea kutekeleza mkakati wa muda mrefu wa kuwawezesha vijana, wakiwemo wenye mahitaji maalum, kupitia vikundi vilivyosajiliwa ili kuongeza ushiriki wao katika shughuli za kiuchumi na kuchangia maendeleo ya taifa.

Kauli hiyo imetolewa bungeni na Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Hamis Mwinjuma kwa niaba ya

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Maendeleo ya Vijana, alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Latifa Khamis Juwakali, aliyetaka kufahamu mipango ya Serikali katika kuwawezesha vijana wenye vikundi vilivyosajiliwa pamoja na wenye mahitaji maalum.

Waziri huyo amesema kuwa Serikali imeweka mazingira wezeshi yanayolenga kuongeza fursa za ajira, ujasiriamali na maendeleo ya kijamii na kiuchumi kwa vijana kupitia programu mbalimbali za uwezeshaji.

Amefafanua kuwa uwezeshaji huo unajumuisha utoaji wa mikopo yenye masharti nafuu kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Vijana, pamoja na Programu ya Uwezeshaji Vijana Kiuchumi inayotekelezwa kupitia shilingi bilioni 200 zilizotolewa kufuatia ahadi ya Rais.

Aidha, Serikali inaendelea kutoa mikopo inayotokana na asilimia 10 ya mapato ya ndani ya halmashauri, hatua inayolenga kusaidia vikundi vya vijana kuanzisha na kuendeleza shughuli za uzalishaji mali.

Katika kuimarisha ushiriki wa makundi maalum katika uchumi, Serikali pia inaendelea kutekeleza utaratibu wa kutenga asilimia 30 ya zabuni za umma kwa vijana, wanawake na watu wenye mahitaji maalum ili kuwapa fursa zaidi za kushiriki katika shughuli za biashara na utoaji wa huduma.

Sambamba na hilo, Serikali imeendelea kuunganisha vikundi vya vijana na taasisi za kifedha pamoja na kuimarisha mifumo ya uratibu na utoaji wa taarifa, hatua zinazolenga kuongeza upatikanaji wa mitaji, fursa za biashara na ajira.

Hatua hizo zinaonesha dhamira ya Serikali ya kuhakikisha vijana na watu wenye mahitaji maalum wanapata fursa stahiki za kiuchumi na kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya nchi.


Kama sehemu ya dhamira yake ya kukuza uendelevu wa mazingira na uhifadhi wa mazingira, Standard Chartered Tanzania imeongoza shughuli ya upandaji miti katika Shule ya Sekondari Nianjema, Wilaya ya Bagamoyo.

Shughuli hiyo inaakisi juhudi zinazoendelea za benki katika kuunga mkono hatua za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, kuhamasisha uelewa wa masuala ya mazingira na kuchangia katika uhifadhi wa mifumo asilia ya ikolojia ya Tanzania.

Mpango wa mwaka huu una umuhimu wa kipekee kwani unaadhimisha miaka 20 ya kujitolea kwa wafanyakazi wa Standard Chartered, ukiashiria miongo miwili ya hatua za pamoja, mchango kwa jamii na ushiriki wa wafanyakazi katika shughuli za kijamii na kimazingira.

Tukio hilo liliwakutanisha wafanyakazi wa benki, viongozi wa eneo husika, wanafunzi na wanajamii katika juhudi za pamoja za kuongeza uoto wa kijani na kuimarisha umuhimu wa utunzaji wa mazingira, Kupitia ushiriki huo, benki inalenga si tu kurejesha mazingira bali pia kuhamasisha utamaduni wa uendelevu kwa vizazi vijavyo.

Mpango huo uliongozwa rasmi na wawakilishi wa serikali za mitaa, jambo lililoonesha umuhimu wa ushirikiano kati ya sekta ya umma na sekta binafsi katika kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi na kusukuma mbele vipaumbele vya taifa katika masuala ya mazingira.

Akizungumza kabla ya tukio hilo, Mkuu wa Transaction Banking Tanzania, Busara Raymond, alisema

“Mazingira ni msingi wa uhai wetu ndiyo chanzo cha hewa ya oksijeni tunayopumua, malighafi tunazotegemea na mifumo ya ikolojia inayodumisha maisha. Hii ndiyo sababu uhifadhi wa mazingira ni muhimu sana, na kwa nini Standard Chartered inaendelea kuweka kipaumbele katika mipango inayolinda na kuhifadhi mazingira yetu.”

“Huu ni mwaka wetu wa tano mfululizo kupanda miti Bagamoyo, jambo linalodhihirisha dhamira yetu ya muda mrefu kwa jamii hii. Mwaka jana tulipanda miche 2,000 katika Shule ya Msingi Fukayosi, na tunajivunia kuendelea kujenga juu ya mafanikio hayo, Mbali na upandaji miti, tunaendelea kushiriki kikamilifu katika shughuli nyingine za kujitolea kwa jamii, ikiwemo kikao cha hivi karibuni cha ushauri na uongozi kwa wanafunzi wa Shule ya Sekondari Pugu Boys.”

Tukio hilo pia lilihudhuriwa na Katibu Tawala wa Wilaya (DAS) wa Bagamoyo, jambo lililoonesha ushirikiano imara kati ya sekta ya umma na binafsi katika kuendeleza mipango ya uendelevu wa mazingira.

Kupitia ushirikiano huo, benki imefanikiwa kupanda zaidi ya miti 10,000 katika Wilaya ya Bagamoyo pekee na zaidi ya miti 30,000 katika Mkoa wa Dar es Salaam, hatua iliyochangia kuboresha uendelevu wa mazingira na kuunga mkono malengo ya upandaji miti nchini.

Kwa miaka mingi, benki imekuwa ikitekeleza programu mbalimbali zinazolenga jamii kwa lengo la kuimarisha ustahimilivu dhidi ya athari za mabadiliko ya tabianchi na kuhamasisha maendeleo endelevu.





Rais wa Jamhuri ya  Singapore Mhe.Tharman Shanmugaratnam, amewasili nchini  kwa Ziara ya Kitaifa ya siku tatu, Juni 8-10, 2026.

Katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam akiwa ameambatana na Mwenza wake Mama Jane Ittogi, alilakiwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Mahmoud Thabit Kombo(Mb) ambaye aliambatana na viongozi wengine waandamizi wa serikali akiwemo Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Albert Chalamila  na Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Ndege Tanzania, Mhandisi Peter Ulanga.

Ziara ya Kitaifa ya Rais Tharman Shanmugaratnam, ni ya kwanza kufanywa na Rais wa Singapore tangu kuanzishwa kwa uhusiano wa kidiplomasia 1980. Ziara hii inaashiria hatua muhimu katika kuimarisha ushirikiano wa kidiplomasia, biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na Singapore.

Akiwa nchini Mheshimiwa Rais Tharman atapokelewa rasmi na mwenyeji wake Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,  Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan Ikulu Dar es Salaam na kuwa  na mazungumzo rasmi kuhusu namna ya kuimarisha ushirikiano katika maeneo ya biashara, uwekezaji, uchumi wa kidijitali, maendeleo ya bandari, elimu, mafunzo ya ujuzi, utalii na miundombinu.

Ziara hiyo pia itajumuisha ushiriki katika Jukwaa la Biashara na Uwekezaji kati ya Tanzania na Singapore pamoja na ziara Zanzibar kwa mazungumzo na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi. 

Ziara hiyo inatarajiwa kufungua fursa mpya za ushirikiano wa kiuchumi na kuimarisha uhusiano wa muda mrefu kati ya mataifa hayo mawili kwa manufaa ya wananchi wake.

















Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) kinatarajia kuadhimisha Maadhimisho ya 11 ya Wiki ya Utafiti na Ubunifu kuanzia Juni 9 hadi 11, 2026, katika Kampasi ya Mwalimu Julius Nyerere, huku Waziri wa Madini, Anthony Mavunde, akitarajiwa kuwa mgeni rasmi.

Maadhimisho hayo yatakayowakutanisha watafiti, wabunifu, wanafunzi, sekta binafsi, taasisi za umma na wadau wa maendeleo, yanalenga kuonesha mchango wa utafiti na ubunifu katika kuharakisha maendeleo ya taifa na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Kaimu Naibu Makamu Mkuu wa Chuo anayeshughulikia Utafiti, Profesa Nelson Boniface, alisema maadhimisho ya mwaka huu yataongozwa na kaulimbiu isemayo: "Kutumia Utajiri wa Madini wa Tanzania katika Kukuza Nishati Jadidifu, Mageuzi ya Kidijitali na Usalama wa Jamii."

Alisema kaulimbiu hiyo imechaguliwa kutokana na umuhimu wa madini katika maendeleo ya teknolojia za kisasa ikiwemo Akili Mnemba (AI), vituo vya kuhifadhi taarifa (Data Centres), magari ya umeme na nishati jadidifu.

“Tunataka kuonesha namna Tanzania inaweza kutumia rasilimali zake za madini kuchochea mageuzi ya kidijitali, kuimarisha usalama wa nishati na kukuza maendeleo ya kijamii na kiuchumi,” alisema Profesa Boniface.

Aliongeza kuwa maadhimisho hayo yatahusisha maonesho ya tafiti na ubunifu, mawasilisho ya kitaaluma, makongamano pamoja na majadiliano ya ushirikiano wa kimkakati yatakayowawezesha washiriki kubadilishana maarifa na kujenga mitandao ya kitaaluma na kibiashara.

Kwa mujibu wa UDSM, maadhimisho hayo yatatoa nafasi kwa watafiti na wabunifu kuonesha suluhisho mbalimbali za kisayansi na kiteknolojia zinazolenga kukabiliana na changamoto za maendeleo nchini katika sekta za madini, nishati, kilimo, afya na uchumi wa kidijitali.

Profesa Boniface alisema chuo kinaendelea kutumia maadhimisho hayo kama jukwaa la kuunganisha taaluma, ubunifu na maendeleo ya taifa kwa kuwafikia wananchi, wawekezaji na wadau mbalimbali wa maendeleo.

"Utafiti na ubunifu ni msingi wa maendeleo endelevu. Tunawaalika Watanzania wote kushiriki katika Maadhimisho ya 11 ya Wiki ya Utafiti na Ubunifu UDSM 2026 ili kujionea kazi na mafanikio ya watafiti na wabunifu wetu," alisema.


Na Farida Mangube Morogoro 

Wakazi wa Kitongoji cha Kichangani, Kijiji cha Mamboya katika Kata ya Gairo, Wilaya ya Gairo, wameondokana na changamoto ya muda mrefu ya mafuriko na kukatika kwa mawasiliano baada ya kukamilika kwa mradi wa ujenzi wa daraja na mtaro wa maji wenye thamani ya zaidi ya Shilingi milioni 455.

Mradi huo uliotekelezwa na wakala ya Barabara za vijjini na mjini TARURA umezinduliwa na Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2026, Ndugu Wazo Michael Mwang’onda, umeleta matumaini mapya kwa wakazi wa Kata hiyo waliokuwa wakikabiliwa na adha ya mafuriko yaliyokuwa yanakatiza mawasiliano na kuathiri shughuli mbalimbali za kijamii na kiuchumi, hususani wakati wa masika.

Akisoma taarifa ya Mradi kwa mkimbiza Mwenge wa Uhuru kitaifa Mhandisi Happnes Mbuge kutoka TARURA WIlaya ya Gairo amesema mradi huo  umehusisha ujenzi wa daraja moja, mtaro wa maji wenye urefu wa mita 330 pamoja na gabioni za kuimarisha kingo za mtaro.

Akizungumza mara baada ya kukagua na kulidhishwa na mradi huo kiongozi wa Mbio za Mwenge wa uhuru kitaifa Ndugu Wazo Michael Mwang’onda amesema mradi huo ni sehemu ya jitihada za kuhakikisha wananchi wanapata miundombinu bora inayowezesha maendeleo na kuboresha maisha yao.

“Mwenge wa Uhuru umejionea kazi kubwa iliyofanyika hapa Kichangani. Huu ni mradi wenye manufaa makubwa kwa wananchi kwa kuwa umeondoa changamoto ya mafuriko na kukatika kwa mawasiliano iliyokuwa ikikwamisha shughuli za maendeleo katika eneo hili. Tunawapongeza wote walioshiriki kufanikisha utekelezaji wake,” alisema Mwang’onda.

Ameongeza kuwa maendeleo ya kweli hujengwa kupitia miradi inayogusa maisha ya wananchi moja kwa moja, huku akisisitiza umuhimu wa wananchi kuendelea kuilinda na kuitunza miundombinu hiyo ili iweze kudumu kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.

“Tunapozindua mradi kama huu tunatarajia kuona ongezeko la shughuli za kiuchumi, urahisi wa upatikanaji wa huduma za kijamii na maendeleo ya wananchi kwa ujumla. Jukumu la kuutunza sasa ni la wananchi wenyewe,” alisema.

Mhandisi Simon Masala ni Meneja wa TARURA Wilaya ya Gairo amesema Mradi huo unatarajiwa kuongeza usalama wa makazi ya wananchi, kuboresha huduma za usafiri na usafirishaji, kurahisisha upatikanaji wa huduma za kijamii na kuchochea ukuaji wa shughuli za kiuchumi katika Kitongoji cha Kichangani, Kijiji cha Mamboya na Wilaya ya Gairo kwa ujumla.

Kwa upande wao, wananchi wa Kichangani wameeleza furaha yao baada ya kukamilika kwa mradi huo wakisema umemaliza tatizo ambalo kwa miaka mingi lilikuwa likiwasababishia hasara na usumbufu mkubwa.

Othuma Yusuf ni Mmoja wa wakazi wa Kata hiyo amesema kabla ya ujenzi wa daraja na mtaro huo, mafuriko yalikuwa yakikatiza mawasiliano kati ya Kichangani na maeneo mengine ya Wilaya ya Gairo, hali iliyokuwa ikiathiri biashara, elimu na huduma za afya.

“Tulikuwa tunapata shida kubwa sana wakati wa mvua. Maji yalifurika na kufanya usafiri kuwa mgumu au kukatika kabisa. Wakulima walishindwa kusafirisha mazao yao kwenda sokoni, wafanyabiashara walikosa wateja na hata wagonjwa walipata changamoto ya kufikishwa hospitali kwa wakati. Kwa kweli tulikuwa tunaumia sana,” alisema Othuma.

Naye Jane Joseph amesema changamoto hiyo ilikuwa ikisababisha wananchi wengi kupoteza fursa za kiuchumi kutokana na kushindwa kufikia masoko na maeneo ya biashara kwa wakati.

“Kipindi cha masika kilikuwa kigumu sana kwetu. Wakati mwingine mazao yaliharibika kwa kuchelewa kufikishwa sokoni na biashara nyingi zilisimama kwa sababu ya kukosekana kwa mawasiliano ya uhakika. Mradi huu umetufungua njia mpya ya maendeleo na tunaamini utaongeza kipato cha wananchi wengi,” alisema Jane.

Aliongeza kuwa pamoja na kuimarisha shughuli za kiuchumi, daraja hilo litasaidia wanafunzi kufika shule kwa urahisi na wananchi kupata huduma za afya bila vikwazo vinavyotokana na mafuriko.

Wananchi hao walitoa shukrani kwa Serikali kwa kupeleka fedha zilizowezesha utekelezaji wa mradi huo, wakisema umekuwa mkombozi mkubwa kwa jamii ya Kichangani na maeneo jirani.










Top News