Makamu wa Rais amesema hayo, wakati alipomwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika Mkutano wa Nne wa kuenzi na kuendeleza Urithi wa Hayati Benjamin William Mkapa na Maadhimisho ya Miaka 20 ya Taasisi ya Benjamin Mkapa (BMF), uliyofanyika katika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) Jijini Dar es Salaam. Amesema Vijana ndiyo viongozi wa sekta ya afya wa kesho, watumishi wa afya na watafiti wajao.
Makamu wa Rais amesema Maisha na uongozi wa Hayati Benjamin Mkapa unatoa mafunzo mengi hususani katika usimamizi na uendelezaji wa sekta ya afya nchini kwa kuwa alitambua nafasi ya afya bora katika maendeleo. Ameongeza kwamba, Hayati Benjamin Mkapa katika awamu yake aliweka mkazo katika mapambano dhidi ya UKIMWI, Malaria na magonjwa mengine yanayoambukizwa na yasiyo ya kuambukiza.
Amesema katika uhai wake, Hayati Mkapa aliamini katika kujenga taasisi na alitumia muda wake, nguvu na jitihada zake nyingi kuhakikisha taasisi hizo zinaimarika. Amesema ushahidi upo unaoonesha kuwa taasisi nyingi zilizoasisiwa katika uongozi wake bado zinaendelea kutekeleza majukumu yake ipasavyo.
Makamu wa Rais amesema ni muhimu kiongozi katika sekta ya afya kuelewa uhusiano uliopo kati ya afya na uchumi, siasa, utamaduni, pamoja na muunganiko kati ya mifumo ya afya ya kitaifa na ya kimataifa. Ameipongeza Taasisi ya Benjamin Mkapa kwa kutoa mchango wake kwa sehemu kubwa kuwezesha viongozi katika sekta ya afya.
Halikadhalika, Makamu wa Rais amesema, viongozi wa awamu nyingine akiwemo Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, pamoja na Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, wameendeleza jitihada za kuimarisha sekta ya afya na kupambana na changamoto zake ikiwemo kusimama kidete kuongoza mapambano dhidi ya UVIKO-19 na magonjwa mengine.
Amesema Serikali ya awamu ya sita chini ya uongozi wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuwekeza kwa kiwango kikubwa katika kukuza elimu ya sayansi, hususan katika taasisi za elimu ya juu kupitia programu mbalimbali. Makamu wa Rais amepongeza ushirikiano kati ya Taasisi ya Benjamin Mkapa na Wizara ya Afya katika kuanzisha jukwaa la vijana kujadili ajenda ya rasilimali watu katika sekta ya afya.
Makamu wa Rais amewahimiza vijana kutumia kikamilifu fursa zitokanazo na maendeleo ya teknolojia kama akili unde, tiba kwa njia ya mtandao ,uchambuzi wa takwimu na teknolojia mpya zitakazoendelea kubadilisha tasnia ya afya.
Makamu wa Rais ameunga mkono azma ya kuubadilisha Mkutano huo kutoka mkusanyiko wa mara moja kila baada ya miaka miwili, na kuwa jukwaa kuu la Afrika la fikra za kitaalamu, majadiliano ya sera, ubunifu na kubadilishana maarifa kuhusu nguvu kazi ya afya, litakalofanyika mara moja kila mwaka.
Mkutano huo, umehudhuriwa na Mlezi wa Taasisi ya Benjamin Mkapa ambaye ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, Viongozi mbalimbali wa Serikali, wadau wa maendeleo wa Kitaifa na Kimataifa, wadau wa sekta ya afya pamoja na wananchi.















.jpeg)


.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)


.jpeg)

.jpeg)


.jpeg)



.jpeg)



.jpeg)
.jpeg)


.jpeg)






.jpeg)