Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa - TAKUKURU Mkoa wa Geita, imewafikisha mahakamani watumishi wa umma saba kwa tuhuma za ubadhirifu wa fedha za Serikali zaidi ya Sh milioni 78.

Akizungumza na wanahabari leo Juni 12, 2026, Mkuu wa TAKUKURU Geita amesema watumishi hao walikusanya mapato kupitia mfumo wa LGRCIS kwa kutumia mashine za POS lakini hawakuwasilisha fedha hizo katika akaunti ya Serikali.

"Uchunguzi umebaini watumishi hao walisababisha Serikali kupata hasara ya jumla ya Sh78,875,110/= kinyume na utaratibu," amesema.

Watumishi hao ni: Tatu Jeki Kijungu - Afisa Hesabu Wilaya ya Geita, Sylvanus Ngoya Michael - Mhasibu Wilaya, Ladislaus Katuma Kamhanda - Afisa Mtendaji Kata Nyamalimbe, Melina Damian Buguba - Afisa Uvuvi, Mtani Daniel Yangwe na Allen Michael Kimaro - Makusanya Mapato Manispaa, na Mashalla Charles Nkwande - Afisa Mtendaji Kata Kakubilo.

Baada ya kupata vibali kutoka Ofisi ya Taifa ya Mashtaka, mashauri 7 yamefunguliwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Geita leo kwa nambari ECO.13145/2026 hadi ECO.13153/2026.



 

Wakulima wa zao la pamba kutoka vijiji vya Mbutu, Iyogelo, Ilambakuki, Imalanguzu na Mwamakoma vilivyopo katika Wilaya ya Igunga, Mkoa wa Tabora, wamehamasika kufungua akaunti za benki na kusajili laini za simu ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya kupokea malipo ya mazao yao kwa njia ya kidijitali. Hatua hiyo inalenga kuongeza uwazi, usalama na uharaka wa malipo kwa wakulima.

Wakulima hao wamefungua akaunti kupitia Benki ya NMB pamoja na kusajili laini kupitia mtandao wa simu wa Mixx by Yas, hatua itakayowawezesha kupokea fedha zao kwa urahisi kupitia mifumo ya benki na huduma za kifedha za simu za mkononi.

Zoezi hilo limefanyika kwa kushirikiana na AMCOS za Ngw'ajojabi, Ngw'asabi na Mwamakoma AMCOS, likitekelezwa kufuatia waraka wa Mrajis wa Vyama vya Ushirika unaoelekeza malipo ya wakulima wa pamba kufanyika kupitia akaunti za benki na huduma za fedha kwa njia ya simu badala ya kutegemea fedha taslimu. Lengo ni kuhakikisha wakulima wanapata malipo yao kwa wakati, kwa uwazi na kwa usalama zaidi.

Mwitikio wa wakulima umeendelea kuongezeka siku hadi siku kufuatia juhudi za uhamasishaji zinazoendelea kufanyika katika maeneo mbalimbali. Hadi kufikia Juni 10, 2026, jumla ya wakulima 506 wamejitokeza na kufungua akaunti pamoja na kujiunga na huduma za kifedha za simu, hatua inayoonesha uelewa na utayari mkubwa wa wakulima kupokea mabadiliko ya mfumo wa malipo ya kidijitali.

Aidha, uhamasishaji wa zoezi hilo umefanywa na Mrajis Msaidizi wa Mkoa wa Tabora, Peja Mhoja pamoja na Mrajis Msaidizi (Uhamasishaji), Ibrahim Kadudu, ambao wamekuwa mstari wa mbele kuwahamasisha wakulima kujiunga na mifumo rasmi ya kifedha ili kunufaika na malipo ya kisasa, salama na yenye tija.

Na Janeth Raphael MichuziTv


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amezitaka taasisi za kifedha nchini kubadili mtazamo katika utoaji wa mikopo kwa kuweka mkazo zaidi kwenye uaminifu, historia ya biashara na mwenendo wa miamala ya waombaji, badala ya kutegemea dhamana za mali zinazoonekana pekee.

Akizungumza leo Juni 12, 2026 katika maadhimisho ya miaka 60 ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT) yaliyofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC), Dar es Salaam, Rais Samia alisema wanawake na vijana wengi wamekuwa wakikosa fursa za kifedha licha ya kuwa na biashara zenye mafanikio na uwezo wa kurejesha mikopo.

Ameeleza kuwa sehemu kubwa ya wanawake na vijana hawamiliki mali kama nyumba, viwanja au magari vinavyoweza kutumika kama dhamana, jambo ambalo limeendelea kuwa kikwazo katika kupata huduma za mikopo kutoka taasisi mbalimbali za fedha.

Rais Samia amesema makundi hayo yana rekodi nzuri za biashara, mauzo yanayoonekana na historia ya miamala inayothibitisha uwezo wao wa kuendesha shughuli za kiuchumi kwa mafanikio, hivyo yanastahili kupewa nafasi zaidi ya kupata mitaji.

Amezitaka benki na taasisi nyingine za kifedha kubuni mifumo ya kisasa itakayowezesha kutathmini uwezo wa wakopaji kwa kutumia taarifa za biashara na mwenendo wao wa kifedha ili kuongeza ushiriki wa wanawake na vijana katika uchumi.

Aidha, Rais Samia amesisitiza kuwa uaminifu wa mteja ni rasilimali muhimu inayopaswa kupewa uzito mkubwa katika maamuzi ya utoaji wa mikopo, akionya dhidi ya kuwanyima wananchi fursa kwa sababu ya kutokuwa na mali zinazokubalika kama dhamana za kawaida.

Katika hatua nyingine, amezitaka taasisi za kifedha kuongeza uwazi kwa kuwapatia wananchi taarifa sahihi na za kueleweka kuhusu masharti ya mikopo kabla ya kuingia kwenye mikataba ya ukopaji.

Amesema ni muhimu kwa wakopaji kuelewa kiwango halisi cha mkopo, muda wa marejesho, viwango vya riba na gharama nyingine zote zinazohusiana na mkopo huo ili waweze kufanya maamuzi sahihi ya kifedha.

Rais Samia pia ameeleza kuwa mafanikio ya sekta ya fedha hayapaswi kupimwa kwa idadi ya watu waliounganishwa kwenye huduma za kifedha pekee, bali kwa kiwango ambacho huduma hizo zinachochea ukuaji wa biashara, kuongeza mitaji na kuboresha maisha ya wananchi.

Kauli hiyo inakuja wakati Serikali ikiendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ya kuimarisha ushiriki wa wananchi katika shughuli za kiuchumi na kuweka mazingira bora yatakayowezesha sekta binafsi kuchangia kwa kiwango kikubwa zaidi katika maendeleo ya taifa.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akikagua mabanda ya maonesho katika Maadhimisho ya miaka 60 ya Benki Kuu ya Tanzania yaliyofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC), Jijini Dar es Salaam tarehe 12 Juni, 2026.

Na Janeth Raphael MichuziTv

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, ameielekeza Benki Kuu ya Tanzania (BoT) kuongeza uwezo wa kuchambua na kutambua mapema mwelekeo wa uchumi wa ndani na wa kimataifa ili kusaidia taifa kukabiliana na changamoto pamoja na kunufaika na fursa zinazojitokeza katika mazingira ya uchumi wa dunia yanayobadilika kwa kasi.

Akizungumza katika maadhimisho ya miaka 60 ya Benki Kuu ya Tanzania yaliyofanyika jijini Dar es Salaam leo Juni 12, 2026, Rais Samia alisema dunia inaendelea kushuhudia misukosuko ya kisiasa, kiuchumi na kifedha ambayo imekuwa na athari kubwa kwa upatikanaji wa bidhaa, uthabiti wa masoko ya fedha pamoja na thamani ya sarafu katika mataifa mbalimbali.

Amesema kuwa mabadiliko hayo yamekuwa yakichochea kupanda kwa gharama za maisha, hususan kupitia ongezeko la bei za mafuta katika soko la dunia, hali inayosababisha kuongezeka kwa gharama za uzalishaji, usafirishaji na huduma mbalimbali.

Rais Samia amesema katika kipindi cha sasa, taasisi za fedha za taifa zinapaswa kwenda mbali zaidi ya jukumu la kawaida la kusimamia sera za fedha na kuhakikisha zinakuwa na mifumo madhubuti ya kutambua vihatarishi kabla havijageuka kuwa migogoro inayoweza kuathiri uchumi na ustawi wa wananchi.

Amesisitiza kuwa Benki Kuu inapaswa kujiimarisha katika ukusanyaji wa taarifa, uchambuzi wa takwimu na utabiri wa mwenendo wa uchumi ili iweze kutoa tahadhari za mapema na kusaidia serikali kufanya maamuzi sahihi kwa wakati.

“Katika mazingira ya sasa ya dunia, taasisi za fedha zinatakiwa kuwa na uwezo wa kuona mbele, kutambua mabadiliko yanayokuja na kuchukua hatua za mapema kulinda uchumi wa taifa,” alisema Rais Samia.

Katika hatua nyingine, Rais huyo ameeleza kuwa Tanzania imeendelea kuimarisha usalama wake wa kifedha kwa kutumia rasilimali za ndani, akitaja ongezeko la akiba ya dhahabu ya taifa iliyofikia tani 27.5 zenye thamani ya takribani Shilingi trilioni 10.

Amesema hatua hiyo ni sehemu ya mikakati ya kuimarisha uthabiti wa uchumi na kujenga kinga dhidi ya misukosuko ya kifedha inayoweza kujitokeza katika masoko ya kimataifa.

Rais Samia amebainisha kuwa mafanikio hayo yanaonyesha umuhimu wa kutumia rasilimali za ndani kama nyenzo ya kuimarisha uwezo wa taifa kukabiliana na changamoto za kiuchumi za sasa na zijazo.

Aidha Rais Samia amesema matarajio yake kwa Benki Kuu katika miaka ijayo, akitaka taasisi hiyo ijijenge kuwa chombo chenye uwezo wa kutambua kwa wakati hatari na fursa za kiuchumi kabla hazijaonekana wazi kwa wadau wengine.

Amesema lengo ni kuona BoT ikibadilika kutoka kuwa msimamizi wa mfumo wa fedha pekee na kuwa taasisi yenye mchango mkubwa katika kulinda mustakabali wa uchumi wa taifa kupitia uchambuzi wa kina, ubunifu na utabiri sahihi wa mwenendo wa uchumi.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea zawadi ya Kitabu cha picha za matoleo ya noti kuanzia mwaka 1966-2026, pamoja na Sarafu ya kumbukumbu ya miaka 60 ya Benki Kuu ya Tanzania kutoka kwa Gavana wa Benki hiyo Bw. Emmanuel Tutuba katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC), Jijini Dar es Salaam tarehe 12 Juni, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akihutubia viongozi pamoja na wageni mbalimbali waliohudhuria kwenye Maadhimisho ya miaka 60 ya Benki Kuu ya Tanzania katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC), Jijini Dar es Salaam tarehe 12 Juni, 2026.

 

Na Mwandishi Wetu

Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) imefanya mazungumzo na Kampuni ya Egyptian Holding Company for Silos and Storage (EHCSS) ya nchini Misri ili kuimarisha usimamizi wa ghala, matumizi ya teknolojia za kisasa na kukuza biashara ya bidhaa za kilimo kati ya Tanzania na Misri.

Mazungumzo hayo yamefanyika Juni 11, 2026 kati ya ujumbe wa WRRB ulioongozwa na Mkurugenzi Mtendaji, Asangye Bangu, akiongozana na Meneja wa Mipango Tafiti na Bunifu, Fidelis Temu na Afisa Ubora Anatolius Kabyemela na viongozi wa EHCSS wakiongozwa na Mkurugenzi Mtendaji na Afisa Mtendaji Mkuu wa taasisi hiyo, Dkt.Ashraf Shedeq.

Katika kikao hicho, WRRB imeeleza uzoefu wa Tanzania katika utekelezaji wa Mfumo wa Stakabadhi za Ghala, huku EHCSS ikieleza namna inavyosimamia ghala za kisasa za kuhifadhi nafaka kwa kutumia teknolojia zinazosaidia kulinda ubora, usalama na ufanisi wa mazao.

Pamoja na hayo, Ujumbe wa WRRB pia umetembelea baadhi ya ghala za EHCSS na kujionea mifumo ya kisasa ya uhifadhi na usimamizi wa bidhaa.

Katika kuendeleza ushirikiano huo, taasisi hizo mbili zimekubaliana mambo kadhaa ikiwamo kuandaa makubaliano ya ushirikiano yatakayosaidia kuongeza fursa za bidhaa za Tanzania kuingia katika soko la Misri, kutoa mafunzo ya kitaalam kuhusu usimamizi wa ghala, kubadilishana uzoefu wa matumizi ya teknolojia za kisasa na kuwezesha biashara ndani ya soko la Afrika kupitia Eneo Huru la Biashara la Afrika (AfCFTA).

Ushirikiano huo unatarajiwa kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania katika masoko ya kimataifa na kufungua fursa mpya za biashara na uwekezaji kati ya nchi hizo mbili.

Na Victor Masangu,Kibaha

Diwani wa kata ya Pangani Mhe. John Katele ameahidi kuchangia mifuko 10 ya simenti kwa ajili ya mradi wa ujenzi wa chuo ambacho kitakuwa kinatumika kama madrasa kinachotarajiwa kujengwa katika eneo la mtaa wa vikawe Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha Mkoa wa Pwani.

Mhe. Katele ametoa ahadi hiyo wakati wa halfa fupi iliyoandaliwa maalumu kwa ajili ya kufanya mchango wa harambee kutoka kwa viongozi na wadau mbali mbali kwa lengo la kuweza kusaidia katika suala zima la kuwezesha ujenzi wa chuo hicho cha madrasa kwa watoto.

"Nashukuru nimeweza kualikwa katika halfa hii fupi nikiwa kama diwani wa kata ya Pangani na lengo langu kubwa ni kuendelea kushirikiana bega kwa bega na wananchi wangu katika mambo mbali mbali ya kijamii hususan jambo hili la ujenzi wa chuo cha madrasa na mimi nitachangia mifuko kumi ya simenti,"amebainisha Diwani Katele.

Aidha Diwani huyo amewahimiza watoto hao ambao watakuwa wanakitumia chuo hicho madrasa pindi kitakapokuja kukamailika kuweka misingi imara ya kuwa na upendo na mshikamano wa pamoja ambao utaweza kuwasaidia kufika mbali katika kujifunza mambo mbali mbali yananayohusu masuala ya dini.

Katika hatua nyingine amewaomba wadau mbali mbali na viongozi sambamba na wananchi kujitolea kwa hali na mali katika kuchangia michango mbali mbali ambayo itaweza kusaidia kukamilika kwa chuo hicho cha madrasa ambacho kinatarajiwa kujengwa katika Kata ya Pangani.




Na Janeth Raphael | Michuzi TV

Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) limetoa nafasi ya mwisho kwa vijana waliohitimu elimu ya sekondari ngazi ya Kidato cha Sita mwaka 2026 na kuchaguliwa kujiunga na mafunzo ya JKT kwa mujibu wa sheria, lakini bado hawajaripoti katika makambi waliyopangiwa.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo Juni 12, 2026, jijini Dodoma na Makao Makuu ya JKT, vijana hao wametakiwa kuripoti kuanzia leo hadi Juni 15, 2026 ili kuendelea na mafunzo yao.

Taarifa hiyo imetolewa na Mkuu wa Tawi la Operesheni na Mafunzo JKT, Peter Mnyani, kwa niaba ya Mkuu wa Jeshi la Kujenga Taifa, Rajabu Nduku Mabele.

JKT imeeleza kuwa vijana ambao hawakufanikiwa kufika katika makambi waliyoelekezwa awali wanapaswa kuripoti katika kambi za JKT zilizo karibu na maeneo wanayoishi ili kurahisisha usajili na kuendelea na mafunzo.

Hata hivyo, Jeshi hilo limefafanua kuwa utaratibu huo hauhusishi vijana wanaotakiwa kuripoti katika Kambi ya Makutupora JKT Camp, Kambi ya Ruvu JKT Camp pamoja na Kambi ya Chuo cha Uongozi Kimbiji, ambazo hazijajumuishwa katika mwongozo huo wa kuripoti kwenye kambi zilizo karibu.

JKT imewasisitiza vijana wote husika kutumia fursa hiyo ya nyongeza ya muda kuhakikisha wanaripoti ndani ya kipindi kilichotolewa ili kutimiza wajibu wao wa kujiunga na mafunzo kwa mujibu wa sheria na taratibu zilizowekwa.






Na PamelaMollel, Arusha

Kampuni ya usafiri wa anga ya Pro Flight Ltd Helicopters Tanzania Kenya imeeleza dhamira yake ya kuendelea kutangaza vivutio vya utalii vya Tanzania kupitia huduma za kisasa za helikopta, hatua inayolenga kuongeza idadi ya watalii pamoja na kurahisisha usafiri katika maeneo mbalimbali ya utalii nchini

Akizungumza na vyombo vya habari jijini Arusha, Afisa wa Udhibiti wa Ubora na Usalama wa kampuni hiyo, Julius Ngeno, alisema huduma za helikopta zimekuwa nyenzo muhimu katika kuwawezesha watalii kufika kwa haraka na kwa usalama kwenye maeneo mbalimbali ya vivutio vya utalii ikiwemo Mlima Kilimanjaro, hifadhi za taifa na maeneo mengine yenye mandhari ya kipekee

Alisema Pro Flight imekuwa ikitoa uzoefu tofauti kwa wageni wanaotembelea Tanzania kwa kuwapa fursa ya kuona uzuri wa nchi kutoka angani, jambo linaloongeza thamani ya safari zao na kuwavutia zaidi kutembelea vivutio mbalimbali vya utalii.

“Tunatumia huduma za helikopta si tu kama usafiri, bali pia kama njia ya kutangaza utajiri wa vivutio vya utalii vya Tanzania. Watalii wanapata nafasi ya kuona mandhari ya kuvutia ya hifadhi, milima na maeneo mengine ya asili kwa mtazamo wa kipekee kutoka angani,” alisema Ngeno

Aliongeza kuwa kutokana na ongezeko la mahitaji ya huduma hizo, kampuni imefungua tawi jipya mkoani Kilimanjaro ili kusogeza huduma karibu zaidi na wateja na kuimarisha shughuli zake katika sekta ya utalii

Kwa mujibu wa Ngeno, huduma za Pro Flight zimekuwa zikiwanufaisha watalii wenye ratiba maalumu, wawekezaji pamoja na makundi mengine yanayohitaji usafiri wa haraka na wa uhakika katika maeneo mbalimbali nchini

Mbali na usafiri wa watalii, kampuni hiyo pia imekuwa ikitoa mchango katika shughuli za uokozi na huduma za dharura, hususan kwa wapandaji wa Mlima Kilimanjaro wanaokumbwa na changamoto za kiafya au ajali zinazohitaji msaada wa haraka.

Ngeno alisema ushiriki wa Pro Flight katika maonesho ya Karibu-KiliFair umeipa kampuni hiyo fursa ya kukutana na wadau mbalimbali wa utalii na kuonesha namna teknolojia ya usafiri wa anga inavyoweza kuchochea ukuaji wa sekta hiyo nchini.

Alisema kampuni itaendelea kushirikiana na wadau wa utalii kuhakikisha Tanzania inaendelea kujitangaza kimataifa kama moja ya destinisheni bora za utalii duniani huku ikitoa huduma za kisasa zinazokidhi mahitaji ya watalii wa kizazi cha sasa.





Na MASHAKA MHANDO -TANGA

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeomba kuendelea kwa ushirikiano kati ya Tanzania na Ireland kupitia utekelezaji wa Awamu ya Pili ya Mradi wa Maziwa Faida kuanzia mwaka 2027 hadi 2032, ili kuendeleza mafanikio makubwa yaliyopatikana katika kuimarisha uzalishaji wa maziwa, kuongeza tija na kuboresha maisha ya wafugaji nchini.

Ombi hilo limetolewa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Dkt. Fabian Madele, wakati akifungua rasmi Maonesho ya Ubunifu na Teknolojia katika Sekta ya Maziwa (TALIRI Open Day 2026) yaliyofanyika katika Kituo cha Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI) Kanda ya Mashariki, jijini Tanga.

Akizungumza katika hafla hiyo, Dkt. Madele amesema Mradi wa Maziwa Faida unaotekelezwa kwa ushirikiano kati ya Serikali ya Tanzania kupitia TALIRI na Taasisi ya Maendeleo ya Kilimo na Chakula ya Ireland (TEAGASC), kwa ufadhili wa Serikali ya Ireland kupitia Ubalozi wa Ireland nchini Tanzania, umeleta mageuzi makubwa katika sekta ya maziwa, hususani katika Mkoa wa Tanga.

Dkt. Madele amesema kabla ya kuanza kwa mradi huo, wafugaji wengi walikuwa wakizalisha wastani wa lita 3 hadi 5 za maziwa kwa ng’ombe mmoja kwa siku. Kupitia matumizi ya teknolojia bora za ufugaji, malisho bora, huduma za ugani zilizoimarishwa na mafunzo kwa wafugaji, uzalishaji umeongezeka hadi wastani wa lita 15 kwa ng’ombe mmoja kwa siku katika maeneo mengi yaliyofikiwa na mradi.

“Matokeo haya yanaonesha wazi mchango mkubwa wa utafiti, ubunifu na ushirikiano wa kimataifa katika kuongeza tija, kuboresha kipato cha wafugaji na kuimarisha usalama wa chakula na lishe nchini,” alisema Dkt. Madele.

Aidha, Dkt. Madele amesema kuwa Tanzania kwa sasa inazalisha takribani lita bilioni 4.1 za maziwa kwa mwaka, wakati mahitaji ya taifa yanakadiriwa kufikia lita bilioni 13 kwa mwaka, amesema hali hiyo inaonesha uwepo wa fursa kubwa ya kuwekeza zaidi katika uzalishaji wa maziwa ili kupunguza pengo la mahitaji na kuongeza mchango wa sekta hiyo katika uchumi wa taifa.

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Balozi wa Ireland nchini Tanzania, Bi. Suzanne Keatinge, ameipongeza TALIRI kwa utekelezaji mzuri wa Mradi huo na kuwatambua watafiti, wataalamu wa ugani na wadau wote waliochangia mafanikio ya mradi huo.

Nae Mkurugenzi Mkuu wa TALIRI Prof. Erick Komba, ameishukuru Serikali ya Ireland kwa ufadhili wake na kueleza kuwa mafanikio yaliyopatikana katika utekelezaji wa Awamu ya Kwanza ya Mradi wa Maziwa Faida (2021/2022–2025/2026) yameweka msingi imara wa kuendelea kuleta mabadiliko chanya katika sekta ya maziwa nchini.

Prof. Komba alisema TALIRI itaendelea kuhakikisha kuwa matokeo ya tafiti, ubunifu na teknolojia zilizozalishwa kupitia mradi huo zinawafikia wafugaji wengi zaidi nchini kwa lengo la kuongeza uzalishaji, tija na ushindani wa sekta ya maziwa.

Aliongeza kuwa Mradi wa Maziwa Faida, uliogharimu zaidi ya Euro milioni 3 sawa na zaidi ya Shilingi bilioni 7 za Kitanzania, umenufaisha zaidi ya wanawake na vijana 3,000 katika ukanda wa pwani ya mashariki, hususan Wilaya ya Muheza mkoani Tanga.

Kwa mujibu wa Prof. Komba, mafanikio makubwa ya mradi huo ni pamoja na kufanya tafiti za malisho bora yanayostahimili mazingira ya ukanda wa pwani, kubaini aina bora za ng’ombe wa maziwa, kuwajengea uwezo maafisa ugani, kutoa mafunzo kwa wafugaji, kuimarisha vyama vya ushirika vya wafugaji, kuboresha miundombinu ya utafiti pamoja na kuanzisha mashamba darasa ambayo yamekuwa vituo muhimu vya kujifunzia na kusambaza teknolojia za kisasa za ufugaji wa ng’ombe wa maziwa.

Mradi wa Maziwa Faida unatajwa kuwa mfano bora wa ushirikiano wa maendeleo unaochochea matumizi ya utafiti na ubunifu katika kutatua changamoto za uzalishaji wa maziwa na kuchangia ukuaji endelevu wa sekta ya mifugo nchini Tanzania.









TANGA – Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeomba kuendelezwa kwa ushirikiano kati ya Tanzania na Ireland kupitia utekelezaji wa Awamu ya Pili ya Mradi wa Maziwa Faida kuanzia mwaka 2027 hadi 2032, ili kuendeleza mafanikio yaliyopatikana katika kuongeza uzalishaji wa maziwa, kuboresha tija na kuinua maisha ya wafugaji nchini.

Ombi hilo limetolewa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Dkt. Fabian Madele, wakati akifungua rasmi Maonesho ya Ubunifu na Teknolojia katika Sekta ya Maziwa (TALIRI Open Day 2026) yaliyofanyika katika Kituo cha Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI) Kanda ya Mashariki, jijini Tanga.

Dkt. Madele alisema Mradi wa Maziwa Faida unaotekelezwa kwa ushirikiano kati ya Serikali ya Tanzania kupitia TALIRI na Taasisi ya Maendeleo ya Kilimo na Chakula ya Ireland (TEAGASC), kwa ufadhili wa Serikali ya Ireland kupitia Ubalozi wake nchini Tanzania, umeleta mabadiliko makubwa katika sekta ya maziwa, hasa Mkoa wa Tanga.

Alieleza kuwa kabla ya kuanza kwa mradi huo, wafugaji wengi walikuwa wakizalisha wastani wa lita tatu hadi tano za maziwa kwa ng’ombe mmoja kwa siku. Hata hivyo, kupitia matumizi ya teknolojia bora za ufugaji, malisho ya kisasa, huduma za ugani zilizoimarishwa pamoja na mafunzo kwa wafugaji, uzalishaji umeongezeka hadi wastani wa lita 15 kwa ng’ombe mmoja kwa siku katika maeneo mengi yaliyofikiwa na mradi.

“Matokeo haya yanaonesha wazi mchango mkubwa wa utafiti, ubunifu na ushirikiano wa kimataifa katika kuongeza tija, kuboresha kipato cha wafugaji na kuimarisha usalama wa chakula na lishe nchini,” alisema Dkt. Madele.

Aidha, alisema Tanzania kwa sasa inazalisha takribani lita bilioni 4.1 za maziwa kwa mwaka huku mahitaji ya taifa yakikadiriwa kufikia lita bilioni 13 kwa mwaka, hali inayoashiria uwepo wa fursa kubwa ya kuwekeza zaidi katika sekta ya maziwa ili kupunguza pengo la uzalishaji na kuongeza mchango wa sekta hiyo katika uchumi wa taifa.

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Balozi wa Ireland nchini Tanzania, Bi. Suzanne Keatinge, aliipongeza TALIRI kwa utekelezaji mzuri wa mradi huo na kuwatambua watafiti, maafisa ugani pamoja na wadau mbalimbali waliochangia mafanikio yake.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa TALIRI, Prof. Erick Komba, aliishukuru Serikali ya Ireland kwa ufadhili wake na kueleza kuwa mafanikio yaliyopatikana katika Awamu ya Kwanza ya Mradi wa Maziwa Faida (2021/2022–2025/2026) yameweka msingi imara wa kuendelea kuleta mageuzi chanya katika sekta ya maziwa nchini.

Prof. Komba alisema TALIRI itaendelea kuhakikisha kuwa matokeo ya tafiti, ubunifu na teknolojia zilizozalishwa kupitia mradi huo zinawafikia wafugaji wengi zaidi ili kuongeza uzalishaji, tija na ushindani wa sekta ya maziwa.

Aliongeza kuwa mradi huo uliogharimu zaidi ya Euro milioni 3, sawa na zaidi ya Shilingi bilioni 7 za Kitanzania, umenufaisha zaidi ya wanawake na vijana 3,000 katika ukanda wa pwani ya mashariki, hususan Wilaya ya Muheza mkoani Tanga.

Kwa mujibu wa Prof. Komba, mafanikio mengine ya mradi huo ni pamoja na kufanya tafiti za malisho bora yanayostahimili mazingira ya ukanda wa pwani, kubaini aina bora za ng’ombe wa maziwa, kuwajengea uwezo maafisa ugani, kutoa mafunzo kwa wafugaji, kuimarisha vyama vya ushirika vya wafugaji, kuboresha miundombinu ya utafiti na kuanzisha mashamba darasa yanayotumika kusambaza teknolojia za kisasa za ufugaji.

Mradi wa Maziwa Faida umetajwa kuwa mfano wa mafanikio wa ushirikiano wa maendeleo unaochochea matumizi ya utafiti, ubunifu na teknolojia katika kutatua changamoto za uzalishaji wa maziwa na kuchangia ukuaji endelevu wa sekta ya mifugo nchini Tanzania.






Top News