Kampuni ya HQ Tanzania imetoa msaada wa vifaa tiba kwa watoto wenye ulemavu wanaolelewa na Kituo cha SBHD Foundation, hatua inayolenga kusaidia ustawi na kuboresha maisha ya watoto wenye mahitaji maalum.

Akizungumza baada ya kupokea msaada huo, Mkurugenzi wa SBHD Foundation, Suma Geofrey, alisema vifaa hivyo vitasaidia kuimarisha huduma zinazotolewa kwa watoto hao na kuchangia katika juhudi za kuwawezesha kuishi kwa kujitegemea zaidi.

Alitoa shukrani kwa uongozi wa HQ Tanzania kwa mchango huo, akisema ushirikiano kati ya sekta binafsi na taasisi zinazohudumia makundi maalum una nafasi muhimu katika kuimarisha ustawi wa jamii.

Suma pia alitoa wito kwa wadau mbalimbali na wananchi kuendelea kushiriki katika kusaidia watoto wenye mahitaji maalum kupitia michango na huduma mbalimbali zinazoweza kuboresha mazingira yao ya maisha na kujifunzia.









Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Judith Kapinga, akiwa katika ziara ya kikazi nchini Uturuki Juni 06, 2026, Jijini Istanbul amefanya mazungumzo na Waziri wa Viwanda na Teknolojia wa Uturuki, Mehmet Fatih Kacır pamoja na Waziri wa Biashara wa Uturuki, Ömer Bolat, kwa lengo la kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi na viwanda kati ya nchi hizi mbili.

Mazungumzo na Waziri Kacır yamejikita katika kukuza maendeleo ya viwanda vya kimkakati, kuimarisha matumizi ya teknolojia, pamoja na kuhamasisha uwekezaji katika viwanda rafiki kwa mazingira.

Mhe. Kapinga ameeleza dhamira ya serikali ya kutumia ushirikiano huo kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya mwaka 2050 ya kuwa nchi ya kipato cha kati cha juu kupitia mageuzi ya sekta ya viwanda, huku Uturuki ikiahidi kuendeleza ushirikiano wa kiufundi, kiteknolojia na ubunifu kwenye sekta hiyo.

Kwa upande wa biashara, mazungumzo na Waziri Bolat yamejikita katika kuimarisha mazingira wezeshi ya uwekezaji na kuongeza kiwango cha biashara kati ya Tanzania na Uturuki, ambacho kwa sasa kimefikia takribani Dola za Marekani milioni 354 mwaka 2026, huku lengo likiwa ni kufikia Dola za Marekani bilioni moja.

Pande zote mbili zilikubaliana kuandaa Mkutano wa Tume ya Pamoja ya Biashara utakaofanyika nchini Tanzania mwaka 2026 ili kujadili kwa kina fursa za kibiashara na uwekezaji.

Waziri Kapinga ametumia fursa hiyo kuelezea maeneo ya kimkakati ya uwekezaji nchini Tanzania, yakiwemo viwanda vya chuma, dawa na vifaa tiba, chakula, pamoja na kongani za viwanda vya kijani (green industrial parks), akisisitiza umuhimu wa kuongeza thamani ya malighafi za kilimo na madini ili kukuza ajira na kuongeza mauzo ya bidhaa zilizochakatwa badala ya kuuza malighafi ghafi.

Serikali ya Uturuki imeahidi kuendeleza ushirikiano wa kimkakati na Tanzania kupitia ubadilishanaji wa teknolojia, ujuzi na kuhamasisha sekta binafsi kushiriki kikamilifu katika miradi ya maendeleo ya viwanda.

Aidha, Waziri Kapinga alifanya mazungumzo na Waziri wa Biashara wa Somalia, Gamal Hassan, ambapo walijadili umuhimu wa kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi kupitia biashara na uwekezaji ili kunufaika vema na fursa za soko la Afrika Mashariki. Vilevile, kupitia mazungumzo hayo Mawaziri hao wameazimia kuanzisha makongamano ya biashara yatakayozikutanisha taasisi za serikali, wafanyabiashara na sekta binafsi kujadili kwa pamoja masuala muhimu ya ushirikiano.

Kadhalika, Mawaziri hao walijadili umuhimu wa uanzishwaji wa safari za ndege kati ya Tanzania na Somalia kupitia Shirika la Ndege la Air Tanzania ili kurahisisha usafirishaji na kupanua mtandao wa biashara kati ya nchi hizi mbili. Waziri Kapinga alihitimisha mazungumzo hayo kwa kumshukuru Waziri Hassan na alimuhakikishia utayari wa Tanzania kuimarisha uhusiano na Somalia na aliwakaribisha wawekezaji kutoka nchini humo kuja kuwekeza Tanzania.














-Asema uaminifu unazidi kupungua

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amewataka viongozi nchini wawaelimishe wananchi umuhimu wa kuandikishana mikataba wanapopeana ardhi badala ya kuendelea kufanya hivyo kwa kuaminiana.

"Viongozi mliopo hapa waambieni wananchi hivi sasa masuala ya ardhi wasifanye kwa kuaminiana, wawe wanaandikishana kwa mikataba na tena katika ofisi za kijiji ili watambulike," amesema. 

Ametoa wito huo leo (Jumapili, Juni 7, 2026) wakati akizungumza na viongozi wa kada mbalimbali wa mkoa wa Iringa katika kikao cha majumuisho ya ziara zake kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa huo, mjini Iringa. 

"Ninawasihi wananchi tusiogope kurasmisha mambo yetu kwa sababu uaminifu unaenda unapungua. Tunaporasmisha, tunaepusha migogoro siku za usoni," amesisitiza. 

Waziri Mkuu ametoa rai hiyo kutokana na wingi wa kero zinazojitokeza kwenye mikutano aliyoishaifanya na hasa kwenye sekta ya ardhi. 

Amewataka viongozi wanapotaka kufanya uendelezaji wowote nao pia wahakikishe wanawapa wananchi husika mikataba ili kulinda haki yao.

"Tusichukue maeneo ya watu bila kuwalipa fidia. Kama kuna uendelezaji ni lazima kuwe na mikataba rasmi. Wananchi wa eneo husika wapewe barua za kuonesha utwaaji huo wakati wakisubiri fedha za fidia zipatikane. Liwe ni eneo limetengwa kwa uwekezaji,  ujenzi wa barabara au shule, watu wapewe barua. Ardhi ni jambo rasmi ndiyo sababu presha ya matumizi inazidi kuongezeka."

Wakati huohuo, Waziri Mkuu amewataka watumishi wa umma wanapokuwa kazini wavae vitambulisho vyenye majina yao ili iwe rahisi kuwatambua.

"Watumishi wa umma wavae vitambulisho ili tuwatambue kwa urahisi wale wanaotukwamisha. Tusirasimishe uozo kwenye ofisi zetu. Zipo ofisi utakuta wanaofanya kazi ni asilimia 20 lakini wanaoenda kazini ni asilimia 80. Twendeni tuchape kazi na kila mmoja amsimamie aliyekabidhiwa chini yake."

Ametumia fursa hiyo kumpongeza Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Heri James,  Mwenyekiti wa CCM wa Mkoa huo, Daudi Yassin na viongozi wote kwa kusimamia vizuri shughuli za maendeleo ya mkoa wao.

"Hongereni sana kwa sababu mkoa wenu umetulia. Nimepita majimbo yote saba sijakutana na ghasia za kugombea nafasi za uongozi. Katika maeneo yote, watu wenu wanaongelea masuala ya maendeleo."

Amesema wakati wa ziara zake, kuna baadhi ya hoja ziliibuliwa na wananchi lakini viongozi wa wilaya na mkoa walikuwa tayari wameshachukua hatua na hata ilipobidi mtu asafirishwe hawakusita kufanya hivyo.

Waziri Mkuu alianza ziara za mkoa wa Iringa Mei 2, mwaka huu kwa kutembelea Halmashauri zote tano na majimbo yote saba kila alipopata nafasi za mwisho wa wiki na leo amefanya majumuisho ya ziara zake. 




Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo, amesema ziara ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, nchini Urusi imefanikiwa kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi na maendeleo kati ya Tanzania na Urusi katika maeneo tisa ya kimkakati yanayotarajiwa kuchochea ukuaji wa uchumi na ustawi wa wananchi wa pande zote.

Akizungumza na waandishi wa habari Juni 7, 2026 jijini Dar es Salaam, Prof. Mkumbo alieleza kuwa Tanzania na Urusi zimeendelea kudumisha uhusiano wa kirafiki wa muda mrefu, huku ziara ya Rais Samia ikifungua ukurasa mpya wa ushirikiano katika sekta mbalimbali muhimu.

Profesa Kitila alitaja maeneo ya ushirikiano kuwa ni pamoja na kilimo, elimu na mafunzo, nishati, madini, viwanda, usafiri, utalii, uchumi wa kidijitali, biashara na uwekezaji na kuongeza kuwa hatua za utekelezaji wa ushirikiano huo zimeanza kuzaa matunda, ambapo makubaliano kadhaa yalifikiwa kati ya taasisi za Tanzania na Urusi kwa lengo la kuimarisha mahusiano na kubadilishana utaalamu katika nyanja mbalimbali.

Alitaja makubaliano husika kuwa ni ushirikiano kati ya Baraza la Kiswahili la Taifa (BAKITA) na Chuo Kikuu cha MGIMO cha Urusi, unaolenga kuendeleza na kukuza matumizi ya lugha ya Kiswahili nchini Urusi ambapo Kiswahili kinatarajiwa kufundishwa kwa kiwango kikubwa zaidi katika taasisi za elimu nchini Urusi.

Profesa Kitila amesema katika mfumo wa kubadilishana tamaduni na lugha, lugha ya Kirusi pia inatarajiwa kuanza kufundishwa nchini na hivyo kuchangia kuimarisha mawasiliano, elimu na uhusiano wa watu wa mataifa hayo.

Amesisitiza kuwa ushirikiano huo unaonesha dhamira ya Tanzania ya kuendelea kujenga uhusiano wa kimkakati na mataifa mbalimbali duniani kwa lengo la kuvutia uwekezaji, teknolojia, maarifa na fursa za maendeleo zitakazowanufaisha wananchi na uchumi wa taifa kwa ujumla.












SERIKALI kupitia Waziri wa Nchi,Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji Profesa Kitila Mkumbo na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mahmoud Thabit Kombo wameeleza namna ziara ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan nchini Urusi ilivyofungua fursa mpya za uwekezaji, biashara na ushirikiano wa kimataifa katika sekta mbalimbali za maendeleo.

Wamesema pia Rais Samia akiwa nchini Urusi ameshiriki katika Jukwaa la Kimataifa la Uchumi la St. Petersburg (SPIEF 2026), ambapo ametumia jukwaa hilo kuendelea kuiweka Tanzania katika ramani ya mataifa yenye mvuto mkubwa wa uwekezaji duniani, jambo ambalo limeongeza matumaini ya ukuaji wa uchumi na ajira kwa Watanzania.

Jukwaa hilo ambalo hushirikisha viongozi wa serikali, wawekezaji wakubwa na wafanyabiashara kutoka mataifa mbalimbali duniani, limeipa Tanzania nafasi adhimu ya kutangaza vivutio vyake vya uwekezaji katika sekta za utalii, madini, kilimo, afya, miundombinu, nishati na teknolojia.

Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari leo Juni 7,2026 jijiji Dar es Salaam alipokuwa akitoa mrejesho kuhusu ziara ya Rais Samia nchini Urusi, Waziri Profesa Mkumbo amesema utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 unahitaji ushirikiano wa wadau kutoka ndani na nje ya nchi, jambo ambalo linaifanya Tanzania kuendelea kutafuta washirika wa maendeleo na uwekezaji duniani kote.

Kwa mujibu wa Prof. Mkumbo amesema ziara hiyo ilikuwa ya kiuchumi zaidi, ikilenga kuvutia uwekezaji, teknolojia na masoko mapya yatakayosaidia kuongeza kasi ya ukuaji wa uchumi wa taifa na kuinua ustawi wa wananchi.

Amesema Tanzania na Urusi zimekubaliana kushirikiana katika maeneo tisa muhimu ambayo ni utalii, kilimo, madini, elimu, sayansi na teknolojia, biashara, uwekezaji, usafirishaji pamoja na uchumi wa kidijitali.

Aidha, amesema tayari makubaliano mbalimbali yameshasainiwa kati ya taasisi za Tanzania na Urusi katika maeneo ya elimu, uwekezaji na biashara, hatua ambayo itaongeza ushirikiano wa moja kwa moja kati ya sekta binafsi za nchi hizo mbili.

Ameongeza banda la Tanzania katika jukwaa hilo lilifanikiwa kuvutia mamia ya wawekezaji waliotaka kupata taarifa kuhusu fursa zilizopo nchini, huku sekta za madini, utalii, uzalishaji wa dawa, mbolea na miundombinu zikitajwa kuwa miongoni mwa maeneo yaliyoonesha mvuto mkubwa.

Kwa upande wake, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mahmoud Thabit Kombo, amesema ziara hiyo imeendelea kuionesha Tanzania kama taifa lenye nafasi muhimu katika diplomasia ya kimataifa kupitia siasa, uchumi na biashara.

Balozi Kombo amesema ushiriki wa Rais Samia katika jukwaa hilo umeongeza ushawishi wa Tanzania duniani, huku ukifungua fursa mpya za masoko ya bidhaa za Tanzania katika mataifa mbalimbali.

Pia amesema hatua ya Rais Samia kutumia lugha ya Kiswahili katika majukwaa ya kimataifa imeendelea kuitangaza Tanzania duniani na kuongeza hadhi ya lugha hiyo kama sehemu ya diplomasia ya utamaduni.

Awali Mkurugenzi wa Biashara ya Kimataifa na Diplomasia ya Uchumi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi John Ulanga amesema Tanzania imepata matokeo makubwa kupitia ushiriki wake katika jukwaa hilo kutokana na ongezeko la wawekezaji na wafanyabiashara walioonesha nia ya kuwekeza nchini.

Amesema pia hotuba ya Rais Samia aliyoitoa katika jukwaa hilo alianza kwa kutumia dakika tatu kuitangaza nchi ya Tanzania kwa kutaja vivutio vya utalii ukiwemo Mlima Kilimanjaro pamoja na hifadhi za taita za utalii kama hifadhi ya Serengeti na baada ya Rais kuinadi Tanzania watu wengi wa nchi ya Urusi pamoja na washiriki wengine wamepata shauku ya kutaka kufika Tanzania.

Aidha amesema sekta za utalii, afya, madini ya kimkakati, teknolojia ya kilimo, uzalishaji wa dawa, usindikaji wa mazao na mbolea ni miongoni mwa maeneo yaliyovutia wawekezaji wengi kutoka Urusi na mataifa mengine yaliyoshiriki jukwaani hapo.

Amebainisha kuwa Tanzania pia imefanikiwa kufungua mazungumzo kuhusu safari za moja kwa moja za watalii kutoka Urusi kuja nchini, hatua inayotarajiwa kuongeza idadi ya watalii na mapato yatokanayo na sekta ya utalii.

Kwa ujumla, ziara ya Rais Samia nchini Urusi imeendelea kuonesha namna Tanzania inavyozidi kujijengea nafasi katika uchumi wa dunia kupitia diplomasia ya uchumi, huku ikifungua ukurasa mpya wa ushirikiano wa kimataifa wenye manufaa kwa maendeleo ya taifa.

Na Mwandishi wetu - Dar es Salaam

Kiongozi Mkuu wa dini ya Buddha nchini, Mchungaji Dkt. Ilukuptiye Pannasekara, amesifu ushirikiano ambao wanaupata sio tu kutoka katika dini zingine bali pia serikalini kwa ujumla.

Ametoa kauli hiyo wakati wa kusherehekea siku ya kuzaliwa kwa kiongozi wa dhehebu la Buddha duniani na uzinduzi wa sanamu ya dhahabu ya Buddha (Golden Buddha Statue) eneo la Upanga jijini Dar es Salaam Juni 7, 2026, ambapo mgeni rasmi alikuwa ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Deus Sangu, akimwakilisha Waziri Mkuu, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba.

Alisema, amekuwa akipata ushirikiano mkubwa kutoka dini nyingine hapa nchini na hivyo kuwafanya waumuni wa Buddha kujisikia furaha.

“Kutokana na mazingira hayo mazuri, tuna jumla ya miradi mitano kwenye sekta za elimu, utalii na afya, miradin hii tayari mingine imeanza na mingine iko katika hatua mbalimbali.” Alisema.

“Hatuhitaji usaidizi wa fedha kutoka serikalini, tunahitaji ushirikiano, miradi hii mitano ni ya uhakika, italeta zaidi ya dola za kimarekani milioni 100 kwenye uchumi wa Tanzania, alisema Mchungaji Dkt. Pannasekara.

Kwa upande wake, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu, amewahakikishia kuwa Serikali ya awamu ya sita chini ya uongozi wake, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, itaendelea kutoa ushirikiano kwa dini zote bila kuwepo kwa ubaguzi.

Amesema Muelekeo wa serikali inapoanza utekelezaji wa dira ya Maendeleo ya 2050 imefungua milango ya kidiplomasia ili kuwaalika wawekezaji kuwekeza hapa nchini.

“Kama serikali tumewahakikishia kuwa kupitia Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji tumewahakikishia kwamba watakapokuwa tayari tutawepeleka kwenye maeneo ya kimkakati ili kutekeleza miradi yao katika sekta za Utalii, Afya na Elimu.” Alisema.



Nchini Tanzania, wabunifu na wajasiriamali wanaendelea kubuni suluhisho mbalimbali ili kukabiliana na changamoto kubwa zinazoikabili mifumo ya chakula nchini, kuanzia uhaba wa maji unaoathiri uzalishaji wa chakula mpaka upatikanaji mdogo wa vyakula vyenye lishe kwa watoto wadogo.

Ili kusaidia kukuza na kuongeza uwezo wa suluhisho hizi zinazoongozwa na wabunifu wa ndani, Shirika la Mpango wa Chakula Duniani (WFP), kwa kushirikiana na StartHub Africa, limezindua IGNITE Challenge Tanzania 1.0 — shindano la ubunifu linalolenga kutambua na kusaidia biashara pamoja na wabunifu wenye uwezo mkubwa wanaofanyia kazi suluhisho endelevu za mifumo ya chakula.

Shindano hili linaangazia maeneo mawili muhimu: suluhisho za matumizi bora ya maji katika uzalishaji wa chakula na vyakula vya nyongeza vyenye lishe kwa watoto wenye umri wa miezi 6 mpaka miezi 59.

Mpango huu unazialika kampuni changa au ‘startups’, biashara ndogo na za kati, wabunifu, na taasisi mbalimbali kuendeleza suluhisho zinazoweza kukua na kutekelezeka kwa vitendo ili kuongeza ustahimilivu kwa jamii, kuimarisha mifumo ya chakula ya ndani, na kuongeza upatikanaji wa lishe.

Kwa mujibu wa WFP Tanzania, lengo la shindano hili siyo tu kutambua mawazo ya kibunifu, bali pia kusaidia suluhisho zenye uhalisia wa kutekelezwa na kukua kwa kiwango kikubwa zaidi.

Washiriki watakaochaguliwa watanufaika na mafunzo ya kitaalamu, msaada wa maendeleo ya biashara, fursa za kuunganishwa na wadau wa mfumo wa ubunifu, pamoja na ufadhili wa mpaka Dola za Kimarekani 40,000 (zaidi ya Shilingi Milioni 100 za Kitanzania) kwa ajili ya hatua ya awali ya ukuaji na kuimarisha ubunifu wao.

Akizungumza kuhusu mpango huo, Mkuu wa Ubunifu wa WFP Tanzania, Tayamika Mattao, alisema IGNITE Challenge inaonesha umuhimu unaozidi kukua wa ubunifu unaoongozwa na wadau wa ndani katika kukabiliana na changamoto za mifumo ya chakula na mabadiliko ya tabianchi nchini Tanzania.

“Nchini Tanzania tunaendelea kuona wabunifu wakibuni suluhisho zenye manufaa makubwa kwa jamii, hasa katika sekta za kilimo, lishe, na ustahimilivu dhidi ya mabadiliko ya tabianchi. Kupitia IGNITE Challenge, tunataka kutengeneza fursa kwa wabunifu hawa kupata msaada, ushirikiano, na rasilimali zinazohitajika ili kukuza mawazo yao na kuchangia katika kujenga mifumo ya chakula iliyo imara na endelevu zaidi,” alisema Bi. Mattao.

Shindano hili linakuja katika kipindi ambacho Tanzania, kama ilivyo kwa mataifa mengi duniani, inaendelea kukabiliwa na athari zinazoongezeka za mabadiliko ya tabianchi zinazoathiri mifumo ya uzalishaji wa chakula, sambamba na changamoto za lishe kwa makundi yaliyo hatarini, hasa watoto walio chini ya miaka mitano.

Kwa wabunifu wanaoendeleza suluhisho za kilimo zinazotumia maji kwa ufanisi ili kuimarisha mifumo endelevu ya chakula katika shule na kambi za wakimbizi, kuboresha upatikanaji wa maji, kuongeza ufanisi wa umwagiliaji, pamoja na uzalishaji wa chakula unaozingatia mabadiliko ya tabianchi, IGNITE Challenge inatoa fursa ya kujaribu, kuboresha, na kukuza suluhisho zao kwa manufaa mapana zaidi.

Vilevile, wazalishaji au wasambazaji wa vyakula wenye uwezo wa kuzalisha vyakula vyenye lishe kwa watoto wenye umri wa miezi 6 mpaka miezi 59 wanahamasishwa kutuma maombi yao ili kusaidia kuboresha matokeo ya lishe kwa watoto nchini Tanzania.

Mpango huu pia unaonesha mwelekeo unaokua wa mifumo ya ubunifu inayoongozwa na wadau wa ndani, ambapo wajasiriamali, taasisi za utafiti, wadau wa maendeleo, pamoja na sekta binafsi wanashirikiana kutengeneza suluhisho zinazokidhi mahitaji halisi ya jamii.

Kupitia shindano hili, WFP kwa kushirikiana na StartHub Africa inalenga kuimarisha mfumo wa kukuza ubunifu na kusaidia biashara zenye matumaini ya kuchangia mifumo endelevu na imara ya chakula nchini Tanzania.

Maombi ya kushiriki kwenye shindano la IGNITE Challenge Tanzania 1.0 yamefunguliwa rasmi.

Waombaji wanatakiwa kutuma maombi yao kabla ya Ijumaa, tarehe 12 Juni 2026, kupitia:

Suluhisho za matumizi bora ya maji katika uzalishaji wa chakula, maombi yatumwe kupitia tovuti ya: www.starthubafrica.org/ignite


Vyakula vya nyongeza vyenye lishe kwa watoto wenye umri wa miezi 6–59, maombi yatumwe kupitia tovuti ya: www.starthubafrica.org/ignite





Na Janeth Raphael MichuziTv - Bungeni Dodoma

Serikali imeendelea kuimarisha hatua za kudhibiti na kutokomeza tatizo la mbegu feki nchini kupitia mifumo ya kisasa ya uthibitishaji wa ubora, ukaguzi wa mara kwa mara na utoaji wa elimu kwa wakulima.

Akijibu swali la Mbunge wa Mbozi, Onesmo Merdson Mnkondya, kuhusu mpango wa Serikali wa kukomesha mbegu feki nchini, Naibu Waziri wa Kilimo, David Silinde amesema kuwa kwa mujibu wa Kifungu cha 15 cha Sheria ya Mbegu (Sura ya 308, Toleo la Urekebu la mwaka 2023), mbegu zote zinazouzwa nchini zinapaswa kuthibitishwa ubora wake na Taasisi ya Uthibitishaji wa Mbegu Tanzania (TOSCI).

Silinde ameaema kuwa TOSCI imeanzisha matumizi ya lebo za kielektroniki zinazotolewa kwa kampuni za mbegu ili kuwasaidia wakulima kuhakiki uhalisia wa mbegu wanazonunua. Kupitia mfumo huo, mkulima anaweza kukwangua lebo maalum iliyowekwa kwenye kifungashio cha mbegu na kuingiza namba husika kwenye simu yake ya mkononi ili kupata taarifa za uthibitisho wa mbegu hizo.

Matumizi ya teknolojia hiyo yameleta mafanikio makubwa katika mapambano dhidi ya mbegu feki, ambapo matukio yaliyoripotiwa yamepungua kutoka 325 mwaka 2014/2015 hadi kufikia matukio 10 pekee mwaka 2023/2024.

Mbali na matumizi ya teknolojia, Serikali kupitia TOSCI inaendelea kufanya ukaguzi wa mara kwa mara katika maduka yanayouza mbegu nchini. Katika ukaguzi uliofanyika kati ya Julai 2025 na Januari 2026, wafanyabiashara 13 walibainika kujihusisha na uuzaji wa mbegu feki au mbegu zisizokidhi viwango vya ubora.

Kwa mujibu wa Waziri, kesi moja tayari ipo mahakamani huku uchunguzi dhidi ya watuhumiwa wengine 12 ukiendelea ili hatua za kisheria ziweze kuchukuliwa.

Aidha, Serikali imeendelea kutoa elimu kwa wakulima kuhusu umuhimu wa kutumia mbegu bora na namna ya kutambua mbegu feki. Kupitia Kampeni ya Mali Shambani, wakulima 5,822 walipatiwa elimu hiyo, huku wakulima wengine 6,763 wakipata huduma na ushauri kupitia Kituo cha Huduma kwa Wateja (Call Center) katika kipindi cha Novemba 2025 hadi Januari 18, 2026.

Silinde amesitiza kuwa Serikali itaendelea kuimarisha usimamizi wa sekta ya mbegu ili kuhakikisha wakulima wanapata mbegu bora na salama, sambamba na kuwalinda dhidi ya wafanyabiashara wanaojihusisha na uuzaji wa mbegu feki.




 Minister of State in the President's Office (Planning and Investment), Professor Kitila Mkumbo, addressing members of the press on the outcomes of the State Visit by the President of the United Republic of Tanzania, Her Excellency Dr Samia Suluhu Hassan, to Russia from 2–6 June 2026. The briefing was held at the Julius Nyerere International Convention Centre, Dar es Salaam, on 7 June 2026.

By Our Correspondent, TBN, Dar es Salaam


Eight signed agreements and memoranda of understanding have laid the cornerstone of a sweeping new partnership between Tanzania and Russia — one that promises to reshape the two nations’ economic, social and technological ties in ways that will be felt for years to come.


The agreements, the direct harvest of President Samia Suluhu Hassan’s historic state visit to Russia, span nine priority sectors: agriculture, education, energy, mining, industry, tourism, transport, the digital economy, and trade and investment — a breadth of ambition that signals a relationship moving well beyond ceremony.


Minister of State in the President’s Office for Planning and Investment, Professor Kitila Mkumbo, laid out the substance of each agreement in full.


From Language Diplomacy to a Revolution in Health and Higher Education


The first agreement turns language itself into a diplomatic instrument. Through a cooperation framework between Tanzania’s National Kiswahili Council (BAKITA) and Russia’s prestigious MGIMO University, the teaching of Kiswahili in Russia will be accelerated, while Tanzania, through the University of Dodoma, prepares to introduce Russian language instruction at home.


The second agreement anchors the partnership in healthcare. The Muhimbili University of Health and Allied Sciences (MUHAS) has entered a formal alliance with two Russian medical institutions, aimed at exchanging specialist expertise and bolstering local pharmaceutical production.


On the education front, the third and fourth agreements address two of Tanzania’s most pressing challenges — graduate employability and technological capability. 


The two countries’ Ministries of Education have signed a mutual recognition agreement for academic certificates and qualifications earned in Russia, a practical step that will allow Tanzanians educated there to enter the local job market without bureaucratic obstruction. 


Meanwhile, the Dar es Salaam Institute of Technology (DIT) has signed an agreement with Russia’s Peoples’ Friendship University to establish joint undergraduate and postgraduate programmes in some of the world’s most sought-after disciplines: Data Science, Aerospace Systems, Artificial Intelligence and Machine Learning.


Attracting Western Capital, Energy Secrets and Opportunities for Youth


The fifth and sixth agreements are designed to unlock significant capital flows. Through the Tanzania Investment and Special Economic Zones Authority (TISEZA), Tanzania gains a platform to attract investment that reaches beyond Russia into the broader European market. 


The partnership with Russia’s Roscongress — a leading organiser of major international business forums — is specifically designed to generate joint ventures and draw interest not only from Russian investors but from Western capitals as well.


The seventh agreement touches a more sensitive register. TANESCO, Tanzania’s national power utility, and Mantra Tanzania Ltd — a subsidiary of Russia’s state nuclear corporation Rosatom — have signed a confidentiality and information protection agreement covering strategic energy projects, a framework that typically precedes deeper operational collaboration.


As a capstone, the eighth agreement is a five-year economic programme explicitly designed to generate employment opportunities for young Tanzanians in Russia — a recognition that the partnership must deliver tangible results at the level of the individual citizen.


“These are the genuine economic fruits of the vision of Her Excellency the President,” Professor Mkumbo said, underlining that the agreements’ implementation is set to leave a lasting mark on Tanzania’s investment landscape and labour market alike.


*TBN stands for Tanzania Bloggers Network


Na Seif Mangwangi, Michuzi TV, Arusha,

MAHAKAMA ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu imesema Tanzania imekuwa  ikikiuka baadhi ya haki za msingi za binadamu kwa  kuendelea kutumia adhabu ya kifo ya lazima na utekelezaji wake kwa njia ya kunyongwa.

Hayo yameelezwa Juni5, 2026 Jijini Arusha na majaji wa Mahakama ya Haki za Binaadam na Watu, (AfCPHR), wakiongozwa na Rais wa Mahakama hiyo Jaji Blaise Tchikaya walipokuwa wakisoma hukumu ya kesi nne zilizowasilishwa mahakama hapo  ikiwemo  shauri lililofunguliwa na wafungwa watatu waliohukumiwa kifo kwa kosa la mauaji.

Aidha Mahakama hiyo imewamuru waombaji watatu katika shauri hilo kulipwa fidia ya Shilingi 300,000 kila mmoja kwa madhara ya kimaadili yaliyotokana na ukiukwaji wa haki zao.

 Uamuzi huo umeonyesha Serikali ya Tanzania ilishindwa kutekeleza wajibu wake wa kulinda na kuheshimu haki za binadamu katika eneo la utoaji na utekelezaji wa adhabu ya kifo kwa mujibu wa viwango vya kimataifa vya haki za binadamu.

Hukumu hiyo ilitolewa mjini Arusha katika kesi iliyowahusisha Godfrey Gabinus Ndimba na wenzake wawili dhidi ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambapo waombaji hao walikuwa wamefungwa katika Gereza la Wilaya ya Lindi wakisubiri utekelezaji wa adhabu ya kifo baada ya kutiwa hatiani kwa kosa la mauaji.

Katika maombi yao, waombaji hao walidai kuwa haki zao zilikiukwa wakati wa uchunguzi, usikilizwaji na utoaji wa hukumu katika mahakama za ndani. Walieleza kuwa kulikuwa na kasoro mbalimbali zilizowaathiri katika kupata haki stahiki.

Mahakama hiyo ya Afrika ilibaini kuwa Serikali ya Tanzania haikuwasilisha majibu yoyote katika shauri hilo licha ya kupewa taarifa zote muhimu na muda wa kutosha kufanya hivyo na  kutokana na hali hiyo, Mahakama iliamua kutoa hukumu kwa kutokuwepo kwa upande wa Serikali.

Kabla ya kuamua shauri hilo, Mahakama ilijiridhisha kuwa ilikuwa na mamlaka ya kusikiliza kesi hiyo na kubaini kuwa madai yaliyowasilishwa yalihusu haki zinazolindwa chini ya Mkataba wa Afrika wa Haki za Binadamu na Watu pamoja na mikataba mingine ya kimataifa iliyoridhiwa na Tanzania.

Mahakama pia ilikubaliana kuwa waombaji walikuwa wametumia njia zote za ndani za kutafuta haki, ikiwemo kukata rufaa katika Mahakama ya Rufani ya Tanzania kabla ya kufikisha shauri lao katika Mahakama ya Afrika.

Katika uchambuzi wa madai ya ukiukwaji wa haki ya kusikilizwa kwa haki, Mahakama ilibaini kuwa waombaji hawakuwasilisha ushahidi wa kutosha kuthibitisha madai yao kuhusu kutengenezwa kwa ushahidi, uwakilishi wa kisheria na mwenendo wa kesi zao. Kutokana na hali hiyo, madai hayo yalitupiliwa mbali.

Kadhalika, madai ya ukiukwaji wa haki ya usawa mbele ya sheria yalikataliwa baada ya Mahakama kubaini kuwa hayakuungwa mkono na ushahidi wa kutosha kuthibitisha kuwa waombaji walitendewa tofauti au kunyimwa ulinzi sawa wa kisheria.

Hata hivyo, Mahakama ilikubaliana na hoja kwamba utoaji wa adhabu ya kifo kwa lazima bila kuzingatia mazingira ya kila mshtakiwa ni ukiukwaji wa haki ya kuishi inayolindwa chini ya Kifungu cha 4 cha Mkataba wa Afrika wa Haki za Binadamu na Watu.

Mahakama pia ilieleza kuwa utekelezaji wa adhabu ya kifo kwa njia ya kunyongwa ni ukiukwaji wa haki ya utu wa binadamu na heshima ya mtu kama ilivyoainishwa katika Kifungu cha 5 cha Mkataba huo.

Kutokana na maamuzi hayo, Mahakama ilihitimisha kuwa Tanzania ilikiuka wajibu wake chini ya Kifungu cha 1 cha Mkataba wa Afrika wa Haki za Binadamu na Watu. Hata hivyo, Mahakama ilikataa maombi ya kufutwa kwa hukumu za ndani na kuwaachia huru waombaji, huku ikisisitiza kuwa fidia ya Shilingi 300,000 kwa kila mmoja ilikuwa hatua stahiki ya kurekebisha madhara ya ukiukwaji wa haki zilizobainika.





Na Mwandishi Wetu

MKURUGENZI Mkuu wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), Dkt. Immaculate Sware Semesi, amesema uhifadhi wa mazingira ni jukumu la kila mwananchi kwa kuwa athari za uharibifu wa mazingira huathiri moja kwa moja maisha ya binadamu na maendeleo ya taifa.

Dkt. Semesi ametoa kauli hiyo wakati akizungumza na wanafunzi katika kilele cha maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani yaliyofanyika jijini Dodoma.

Amesema NEMC inaendelea kutekeleza mikakati mbalimbali inayolenga kubadili mtazamo wa wananchi kuhusu taka kwa kuzifanya kuwa fursa za kiuchumi kupitia ukusanyaji, uchakataji na uzalishaji wa bidhaa mbalimbali zinazotokana na taka.

Kwa mujibu wa Dkt. Semesi, hatua hiyo inalenga kusaidia kulinda mazingira huku ikiongeza kipato kwa wananchi kupitia shughuli za urejelezaji na uchumi wa mzunguko.

Aidha, amesema NEMC imejipanga kuendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa kulinda na kuhifadhi mazingira ili yaendelee kutoa huduma muhimu za kiikolojia, fursa za kiuchumi na kuchangia maendeleo endelevu ya nchi.

Aliongeza kuwa maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani yamekuwa jukwaa muhimu la kuelimisha umma kuhusu masuala ya mazingira pamoja na kutoa ushauri wa kitaalamu unaolenga kuboresha huduma za usimamizi na uhifadhi wa mazingira nchini.

Dkt. Semesi amewahimiza wanafunzi na wananchi kwa ujumla kushiriki kikamilifu katika shughuli za utunzaji wa mazingira, ikiwemo upandaji miti, usimamizi bora wa taka na matumizi endelevu ya rasilimali za asili ili kuhakikisha mazingira salama kwa kizazi cha sasa na kijacho.

Mkurugenzi Mkuu wa NEC Immaculate Semes akiwa Katika picha ya pamoja kilele cha maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani.
-Wananchi wa zaidi 400 wapata elimu ya uhifadhi wa mazingira kutoka NEMC Dodoma.

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Zaidi ya wananchi na wadau 400 wametembelea banda la Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) na kupata elimu kuhusu uhifadhi wa mazingira katika maadhimisho ya Wiki ya Mazingira Duniani yaliyofanyika jijini Dodoma.

Meneja wa Kanda ya Kati wa NEMC, Novatus Mushi, amesema mwitikio huo unaonesha kuongezeka kwa uelewa wa wananchi kuhusu umuhimu wa kuhifadhi mazingira na mchango wa elimu katika kubadili mitazamo ya jamii kuelekea maendeleo endelevu.

Akizungumza katika kilele cha maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani yaliyofanyika katika Ukumbi wa Jakaya Kikwete Convention Centre (JKCC) Juni 5, 2026, Mushi alisema NEMC imeendelea kutumia mifumo ya kisasa ya kidijitali katika kusimamia na kufuatilia mazingira kwa wakati halisi.

Alisema miongoni mwa mifumo hiyo ni teknolojia inayowezesha kutambua viashiria vya uchafuzi wa mazingira mara vinapotokea, hatua inayorahisisha ufuatiliaji na kuchukua hatua stahiki kwa wakati.

“Tunazo mifumo ya kisasa ya usimamizi wa mazingira ya kidijitali. Mfumo huu mpya unatuwezesha kuona dalili za uchafuzi wa mazingira kwa wakati halisi na hivyo kuongeza ufanisi katika usimamizi wa mazingira,” alisema Mushi.

Aidha, alisema NEMC inaendelea kutumia Mfumo wa Usimamizi wa Miradi (PMS) unaorahisisha utoaji wa vibali vya Tathmini ya Athari kwa Mazingira (EIA) kwa miradi mbalimbali ya maendeleo kabla ya kuanza kutekelezwa.

Kwa mujibu wa Mushi, matumizi ya mifumo hiyo yamechangia kuongeza uwazi, kupunguza muda wa utoaji huduma na kuimarisha usimamizi wa mazingira nchini.

Amesema maonyesho hayo yamewapa fursa wadau na wananchi kujifunza namna teknolojia inavyoweza kutumika katika kulinda mazingira na kuhimiza maendeleo yanayozingatia uhifadhi wa rasilimali za asili.

Mushi pia alisema NEMC inaendelea kushirikiana na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) katika kubadilishana taarifa na takwimu za hali ya hewa na mazingira ili kusaidia kupanga na kutekeleza miradi kwa kuzingatia athari za mabadiliko ya tabianchi.

Alieleza kuwa ushirikiano huo unasaidia kufanya maamuzi sahihi ya maendeleo na kuzuia hasara kubwa za kiuchumi ambazo zinaweza kujitokeza endapo miradi itatekelezwa bila kuzingatia taarifa muhimu za hali ya hewa na mazingira.

Akizungumzia mwelekeo wa NEMC kuwa mamlaka kamili, alisema hatua hiyo itasaidia kuimarisha ufanisi wa utendaji kazi, kupunguza urasimu na kuongeza kasi ya utekelezaji wa majukumu ya usimamizi wa mazingira.

“Mazingira, watu na uchumi lazima viendane. Tukipata mamlaka kamili tutaongeza ufanisi wa utendaji kazi na kuboresha huduma kwa wananchi,” alisema.

Hata hivyo, alisema Kanda ya Kati inayojumuisha mikoa ya Dodoma, Singida na Iringa bado inakabiliwa na changamoto mbalimbali za mazingira, ikiwemo migogoro ya matumizi ya ardhi, matumizi ya teknolojia duni katika shughuli za kiuchumi na uelewa mdogo wa baadhi ya wananchi kuhusu umuhimu wa uhifadhi wa mazingira.

Alisema NEMC itaendelea kuimarisha utoaji wa elimu kwa umma, usimamizi wa sheria za mazingira na ufuatiliaji wa shughuli mbalimbali ili kuhakikisha rasilimali za mazingira zinahifadhiwa kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Mkurugenzi Mkuu wa NEC Immaculate Semes akiwa  Katika picha ya wanafunzi akifanya mazungumzo wanafunzi waliokuwa wakitoa elimu ya uhifadhi wa mazingira katika    kilele cha maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani mjini Dodoma



Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Mussa Azan Zungu ametembelea na kukagua maendeleo ya ujenzi wa Shule ya Sekondari ya Mfano ya Benki ya CRDB (CRDB Bank Secondary Model School) inayojengwa Upanga katika Halmashauri ya Ilala.

Mheshimiwa Zungu aliyepokelewa na Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Benki ya CRDB na Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB Bank Foundation, TullyEsther Mwambapa amepongeza kasi ya mkandarasi na kumuomba akamilishe ujenzi mapema iwezekanavyo ili kuwanufaisha wanafunzi wanaotarajiwa kujiunga.

"Shule hii inajengwa Ilala ila itawahudumia wanafunzi kutoka kila mahali. Nampongeza Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Dkt. Abdulmajid Nsekela na menejimenti nzima kwa kuona umuhimu wa kujenga shule hii itakayowafaa watoto wa Kitanzania. Nikuombe mkandarasi, ongeza kasi ujenzi ukamilike mapema," amesema Spika Zungu.

Akieleza maendeleo ya mradi huo, Tully amesema utakagharimu jumla ya shilingi bilioni 5. "Itakuwa shule bora na ya kisasa. Tunashukuru serikali ya Manispaa ya Ilala kwa kutuamini na kushirikiana nasi kuboresha maisha ya wananchi," amesema Tully.

Kuhusu kukamilika kwa ujenzi huo, Mhandisi Anna Mafoka, mkandarasi anayeujenga mradi huo amesema mkataba ulitaka shule hoyo ijengwe kwa miezi 10 na kukamilika Machi mwakani lakini watajitahidi majengo yawe tayari kwa matumizi ifikapo Desemba ili Januari yaanze kutumika.











Top News