BENKI ya Maendeleo ya Kilimo (TADB), imesema katika kutambua umuhimu wa kusogeza huduma karibu zaidi kwa wadau wake inaendelea na mipango ya kufungua ofisi rasmi ya TADB Zanzibar.

Benki hiyo imesema kwa sasa inatoa huduma zake kwa ngazi ya kanda visiwani Zanzibar kwenye ofisi zilizopo Jengo la ZURA Mtaa wa Maisara.

Ahadi hiyo ilitolewa jana Unguja na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki hiyo, Frank Nyabundege, wakati wa futari na wadau wa Zanzibar ambayo pia ilihudhuriwa na Dk Juma Malik Akili ambaye ni Waziri wa Fedha na Mipango wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ambaye alimwakilisha Mhe.Rais wa Zanzibar, Waziri wa Kilimo, Suleiman Masoud Makame, Waziri wa Nchi ofisi ya Makam wa Pili wa Rais, Sera, Uratibu na Baraza la Wawakilishi Mhe. Hamza Hassan Juma, na Waziri wa Uchumi wa buluu, Masoud Ali.

Alisema hatua ya kufungua ofisi rasmi visiwani Zanzibar itasaidia kuongeza upatikanaji wa huduma za kifedha na ushauri wa kitaalamu kwa wakulima, wafugaji na wavuvi katika kanda ya Zanzibar.

Alisema tangu kuanzishwa kwake, benki ya TADB imeweza kutoa huduma jumuishi za kifedha kwa kutoa mikopo Jumla shilingi bilioni 12.47 kwa Zanzibar, ikijumuisha Unguja na Pemba,

Alsiema Benki imeweza kuchagiza uwekezaji katika miradi 49 katika maeneo makuu ya uwekezaji yalikuwa usindikaji wa mazao ya kilimo (milioni 208), maghala ya kutunza baridi (milioni 4.5).

Alisema ununuzi wa mazao kutoka kwa wazalishaji shilingi bilioni 6.65), umwagiliaji (milioni 175), matumizi ya mitambo ya kilimo (milioni 153), pembejeo za kilimo (bilioni 1.6), mifugo hai (bilioni 1.14) na mikopo kwa wanawake na vijana (bilioni 1.07) na ufadhili wa mali kama vile malori, mabanda na vizimba vya wanyama (bilioni 1.94).

Alisema Benki imewezesha utendaji wa minyororo ya thamani iliyofanya vizuri zaidi ilikuwa karafuu (bilioni 6.54), kuku (bilioni 3.58), na maziwa (bilioni 1.17) na kutaja minyororo mingine ya thamani kuwa ni (mahindi, mpunga, matunda na mboga) ilipokea jumla ya (milioni 420).

Nyabundege alisema TADB imeweza kuwakifia jumla ya wanufaika 571, kati yao wanawake walikuwa 221, wanaume 350, na kati ya wanufaika 571 vijana ni165.

“Mbali na shughuli za utoaji wa mikopo, Benki pia inatambua umuhimu wa kutekeleza wajibu wake kwa jamii kupitia dhana ya uwajibikaji wa kijamii wa taasisi (Corporate Social Responsibility). Katika tukio hili la leo, Benki imeandaa misaada mbalimbali inayotolewa kwa baadhi ya makundi maalum katika jamii,” alisema.

Aidha, alisema misaada hiyo inahusisha pembejeo za kilimo, misaada wa kifedha pamoja na vyakula, iliyolenga kuwasaidia watu wenye mahitaji.

“ Naomba kukujulisha kuwa katika majitoleo yetu Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) tumeweza kukabidhi Misaada mbalimbalj kwa vituo viwili vya watoto wenye mahitaji maalumu hapa Zanzibar,” alisema.

Aidha, alisema Benki imepanga kuchagiza shughuli za Vikundi vya Vijana, Wanawake Pamoja na wanaume kuwawezesha ili kukuza ufugaji na kilimo hapa Zanzibar.

Aliishukuru Serikali kwa kuendelea kuweka mazingira wezeshi yanayowezesha taasisi kama Benki hiyo kuendelea kuwahudumia wakulima, wafugaji na wavuvi nchini.

“Sera na mipango ya Serikali imeendelea kutoa msukumo mkubwa katika kukuza sekta ya kilimo ambayo ni mhimili muhimu wa uchumi wa Taifa letu,” alisema.

“Tunapenda kuendelea kushirikiana kwa karibu na Serikali pamoja na wadau wengine katika kuhakikisha kuwa sekta ya kilimo, ufugaji na uvuvi inaendelea kukua na kuchangia zaidi katika maendeleo ya uchumi na ustawi wa wananchi wetu,” alisema na kuongeza.

“ Tunawashukuru sana kwa kuitikia mwaliko wetu na kuja kushirikiana nasi katika tukio hili la kuimarisha uhusiano na ushirikiano wetu,” alisema Nyabundege









Na FARIDA MANGUBE, MOROGORO

Wanawake wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Morogoro wameungana na wanawake wengine kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani inayoadhimishwa kila ifikapo Machi 8 kila mwaka huku wakisisitiza umuhimu wa wanawake kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya jamii na taifa.

Kwa Mkoa wa Morogoro maadhimisho hayo yamefanyika katika viwanja vya Shule ya Msingi Fulwe, Halmashauri ya Wilaya ya Morogoro, ambapo wanawake wa TRA Mkoa wa Morogoro walishiriki pamoja na wanawake kutoka taasisi na makundi mbalimbali kuadhimisha siku hiyo maalum inayotambua mchango wa wanawake katika nyanja mbalimbali za maendeleo.

Akizungumza wakati wa maadhimisho hayo Meneja Msaidizi Ukaguzi TRA Mkoa wa Morogoro Bi Beatrice Steven amesema kuwa ushiriki wao katika siku hiyo unaonesha dhamira ya taasisi hiyo kuendelea kuunga mkono juhudi za kuwawezesha wanawake na kuhamasisha usawa wa kijinsia katika jamii.

Amesema wanawake wana nafasi kubwa katika kuchangia maendeleo ya kiuchumi ya taifa kupitia majukumu yao mbalimbali ikiwemo katika sekta ya ukusanyaji wa mapato, biashara, elimu na uongozi, hivyo ni muhimu kuendelea kuhamasisha ushiriki wao katika maendeleo.

Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani ni fursa ya kuimarisha mshikamano, kubadilishana uzoefu na kujadili changamoto zinazowakabili wanawake ili kutafuta suluhisho litakalowezesha maendeleo yao na ya jamii kwa ujumla.

Maadhimisho hayo yalipambwa na shughuli mbalimbali zikiwemo maandamano ya amani, burudani pamoja na utoaji wa ujumbe unaohamasisha jamii kuendelea kuthamini mchango wa wanawake katika maendeleo ya taifa.

Siku ya Wanawake Duniani huadhimishwa kila mwaka Machi 8 duniani kote kwa lengo la kutambua mafanikio ya wanawake katika nyanja za kijamii, kiuchumi na kisiasa pamoja na kuendelea kuhamasisha usawa wa kijinsia.






Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dkt. Asha-Rose Migiro, leo Jumatatu,Machi 9,2026, amefungua rasmi mafunzo maalum ya Uongozi na Utawala Bora kwa viongozi na watendaji waandamizi wa Chama yanayofanyika katika Ukumbi wa Mount Royal, Mkoani Iringa.

Mafunzo hayo ya siku nne yameandaliwa na Jitegemee Holdings Company Limited (JHCL) kwa kushirikiana na Taasisi ya Wakurugenzi Tanzania (IoDT), na yanawaleta pamoja wajumbe wa Bodi, Menejimenti ya Jitegemee Holdings pamoja na viongozi waandamizi wa CCM.

Akifungua mafunzo hayo, Dkt. Migiro amesema kuwa uongozi na utawala bora ni msingi muhimu wa kuimarisha taasisi na kuendeleza maendeleo ya Taifa, akisisitiza kuwa mafunzo hayo yanaendana na utekelezaji wa Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu wa 2025 pamoja na maono ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Aidha, amewataka washiriki kutumia fursa ya mafunzo hayo kujenga uwezo wa kiuongozi na kuhakikisha maarifa watakayopata yanatumika kuimarisha utendaji wa taasisi wanazoziongoza.









Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ametoa punguzo la kodi kwa wafanyabiashara wa Soko Kuu la Kariakoo ambapo kwa wafanyabiashara wa vizimba wamepata punguzo la asilimia 17 huku wale wa biashara zingine kama maduka wamepata punguzo la asilimia 10 hadi 16.

Uamuzi huo wa Rais Samia umetangazwa kwa waandishi wa habari na Meneja Mkuu wa Shirika la Masoko ya Kariakoo CPA. Ashraph Abdulkarim ambapo ameongeza kuwa pamoja na punguzo hilo la kodi Mhe. Rais ametoa msamaha wa kodi ya mwezi mmoja tangu alipofungua soko hilo Februari 8,2026 hadi Machi 8, 2026.

“Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suuhu Hassan ameridhia punguzo hilo la kodi kutokana na maombi ya wafanyabiashara waliyoyatoa kwake kutokana na changamoto mbalimbali walizokumbana nazo baada ya soko hili kupata ajali ya moto mwaka 2021, hivyo tunamshukuru Mhe. Rais kwa moyo wake wa usikivu na upendo mkubwa kwa wafanyabiashara” ameongeza CPA. Abdulkarim

Kabla ya kukutana na waandishi wa habari alifanya kikao na viongozi wa wafanyabiashara wa soko hilo ili kuwaeleza uamuazi wa Mhe. Rais ambapo walishukuru kwa uamuzi huo ambao umejali utu na kuwapa hamasa ya kuendelea kufanya biashara na kulipa kodi kwa maendeleo ya taifa.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa wafanyabiashara sokoni hapo, Bw. Ramadhani Kakandilo ameishukuru Serikali kwa kuwajali wafanyabiashara na kuongeza kuwa wataendelea kushirikiana na uongozi wa soko hilo ili mtaji uliowekwa na serikali uwe na manufaa kwa vizazi vya sasa na vijavyo.





Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) leo Machi 9, 2026 imetembelea watoto wenye mahitaji maalum katika vituo viwili vya kulelea watoto Zanzibar kwa lengo la kuwafariji na kuwaunga mkono katika kipindi hiki cha mfungo mtukufu wa Ramadhani.

Katika ziara hiyo, benki ilifika katika Kituo cha ZASO Children Home kilichopo Fuoni Mambo Sasa ambacho kina watoto 47, pamoja na Kituo cha Kulelea Watoto Yatima cha Mssers Markaz Orphanage kilichopo Fuoni Jitimai chenye watoto 83.

Kupitia ziara hiyo, TADB ilikabidhi msaada wa mahitaji mbalimbali muhimu kwa watoto hao ili kuwasaidia katika maisha yao ya kila siku, hususan katika kipindi hiki cha Ramadhani.

Msaada huo ulikabidhiwa rasmi na Meneja wa Kanda ya Zanzibar wa TADB, Bw. Ally Jamal, akiongozana na wafanyakazi wa benki hiyo.

Hatua hiyo inaashiria dhamira ya TADB ya kuendelea kushiriki katika shughuli za kijamii, kuonesha upendo na mshikamano, pamoja na kugusa maisha ya makundi yenye uhitaji maalum katika jamii.













Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika Umoja wa Afrika na Mkuu wa Ofisi ya Umoja wa Mataifa katika Umoja wa Afrika (UNOAU), Bw. Parfait Onanga-Anyanga amewasili nchini kwa ziara akiwa kama Mjumbe Maalum wa Mhe. Antonio Guterres, Katibu Mkuu UN kwenye ziara ya kikazi lengo likiwa ni kukutana na kufanya mazungumzo na Mamlaka pamoja na wadau mbalimbali kuhusu matukio yaliyotokea kabla na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Tanzania, 2025 na kuangalia hali ya maisha ya Tanzania kwa sasa.

Bw. Onanga-Anyanga ametoa pongezi hizo alipofanya mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb.), jijini Dar es Salaam, ikiwa ni hatua ya mwanzo ya mazungumzo yake na Serikali pamoja na wadau mbalimbali wa kitaifa.

Mjumbe huyo yupo nchini kwa ziara ya kikazi kwa lengo la kufanya mashauriano na Serikali na wadau wengine wa kitaifa kuhusu hali ya kisiasa nchini, pamoja na kujadili namna Umoja wa Mataifa unavyoweza kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuimarisha taasisi za kidemokrasia, kusimamia mageuzi na kuendeleza umoja na mshikamano wa kitaifa kupitia maridhiano jumuishi.

Aidha, amempongeza Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuonesha utulivu na uongozi makini katika kipindi hicho kigumu kwa taifa. Amekaribisha pia uamuzi wa Serikali wa kuunda Tume ya Kuchunguza Matukio Wakati na Baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025

Bw. Onanga-Anyanga aliipongeza Tume hiyo inayoongozwa na Mhe. Mohamed Chande Othman, Jaji Mkuu Mstaafu kwa kazi yake nzuri yenye kubeba uzito na ubobezi na viwango vya hali ya juu na ya kuigwa kimataifa. Ameeleza pia kuwa muundo wa Tume hiyo unaojumuisha wajumbe kutoka kada mbalimbali umeongeza ubora na uhuru wa kazi yake.

Aidha, ameipongeza Serikali kwa juhudi zake za kurejesha imani ya wananchi na kudumisha utulivu baada ya matukio hayo, pamoja na hekima na utulivu uliotumika katika kushughulikia changamoto zilizojitokeza wakati wa kipindi cha uchaguzi.

Katika muktadha huo, Mwakilishi huyo Maalum alikaribisha mpango mpana wa kitaifa uliotangazwa na mamlaka mwezi Januari 2026 chini ya kaulimbiu ya “Repair – Rebuild – Renew,” akibainisha kuwa mpango huo unaweka msingi muhimu wa kuimarisha utawala wa kidemokrasia, kusimamia mageuzi ya taasisi pamoja na kuendeleza maridhiano ya kitaifa.

Vilevile, amempongeza Mhe. Mahmoud Kombo, kwa juhudi zake za kuielezea jumuiya ya kimataifa hatua na michakato ya ndani ya nchi inayochukuliwa kushughulikia matukio hayo na kuimarisha mshikamano wa kitaifa.

Katika ratiba ya ziara yake nchini, Bw. Onanga-Anyanga anatarajiwa kukutana na viongozi wa vyama vya siasa ikiwemo Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), ACT Wazalendo, Chama cha Ukombozi wa Umma (CHAUMA) na Chama Cha Mapinduzi (CCM) ili kubadilishana mawazo kuhusu masuala ya utawala bora, demokrasia na mshikamano wa kitaifa.

Aidha, atafanya mazungumzo na Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jaji Mkuu pamoja na Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambani ni wawakilishi wa mihimili yote mitatu ya dola.

Kwa upande wake, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb.) ameishukuru Umoja wa Mataifa kwa ushirikiano wake na kueleza kuwa Tanzania inathamini sana ushirikiano huo. Ameeleza kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na UN na haitasita kuomba msaada wake pale inapohitajika katika kuimarisha taasisi za taifa na kulinda amani, utulivu na mshikamano wa wananchi.














Top News