Na Said Mwishehe,Michuzi TV

ASASI ya AGENDA imesema imeridhishwa na utekelezaji wa mradi wa kuhamasisha wakulima katika Halmashauri ya Manispaa ya Wilaya ya Kigamboni mkoani Dar es Salaam kulima kilimo endelevu ambacho kitasaidia mazingira yawe endelevu na wenyewe wawe na afya bora.

Akizungumza na Waandishi wa habari baada ya kufanya ziara ya ufuatiliaji wa mradi huo ambao pia ulihusisha upandqji wa miche ya miti ya matunda katika mashamba ya wakulima pamoja na shule za msingi na sekondari, Katibu Mtendaji wa AGENDA Dorah Swai amesema wakulima wametekeleza mradi huo kwa kiwango kikubwa.

“Katika mradi huu tulikuwa tunahimiza wakulima kulima kilimo endelevu ambacho kitasaidia mazingira yawe endelevu kwa kulima kilimo ambacho hakitumii kemikali za viwandani zenye sumu za kuulia wadudu maarufu viuatilifu badala yake wameelekezwa jinsi ya kutengeneza viuatilifu vinatenengezwa kwa majani ya miti, miti ,mkojo wa sungura .”

Pia waliekezwa katika mashamba yao wpande miti kwasababu mbalimbali ikiwemo ya kukabiliana na tabianchi huku akieleza walikuwa wakiwahamasisha kupanda miti ya matunda ambayo inafaida nyingi kama chakula na Kivuli.

Ameongeza kwa wanafunzi shuleni AGENDA iliwafundisha kupanda miti kwa lengo la kukabiliana na tabianchi na kupendezesha mandhari ya shule zao .”Walipanda miti ya matunda.”

Aidha amesema pia utekelezaji wa mradi huo unaofanuwa na AGENDA ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za Serikali upatikanaji wa chakula mashuleni kwasababu miti itakapokuwa watoto watapata chakula pamoja na kivuli

“Katika kufuatilia tumeona kuna juhudi kubwa ya walengwa katika kutunza miche ambayo walipewa kuipanda katika kashamba kwani inaendelea vizuri.Tunawashukuru manispaa ya Kigamboni kwani mradi huu hatujautekeleza peke yetu bali na wao tulikuwa nao muda wote.

“Katika kutoa mafunzo kwa Wakulima tumeshirikiana wote na tumekuwa nao katika kila hatua ya utekelezaji wa mradi huu.Mradi huu umetekelezwa kupitia ufadhili wa fedha zilizotolewa na GGF lililopo nchini Marekani,”amesema Swai.

Kwa upande wake Mkuu wa Idara ya Kilimo,Mifugo na Uvuvi katika Halmashauri ya Manispaa ya Wilaya ya Kigamboni mkoani Dar es Salaam Priscila Mhina amesema wamekuwa wakiwasaidia wakulima kwa njia mbalimbali ikiwemo ya kutumia watalaam waliosambazwa kila kata kwa ajili ya kutembelea wakulima kutoa ushauri na kuwaelekeza jinsi ya kulima kilimo bora

Pia amesema wanaunganisha wakulima pamoja na wadau mbalimbali wa kilimo wakiwemo AGENDA ambao wao wamekuja na ajenda muhimu kwa wakulima wetu kwa kipindi hiki.

“Kupitia mradi wa AGENDA tunawahamasisha zaidi wakulima kutumia dawa za asili kukabiliana na tabianchi, kulinda aridhi na mazao kwani kumekuwa na tabia wakulima kutumia dawa zenye kemikali ambazo zinasababisha sumu na ile sumu baadae zinakwenda kumuathiri mtumiaji.

“Sasa AGENDA wamekuja na ajenda yao nzuri ya kutumia dawa asili ambapo tulianza na shamba darasa katika kituo chetu cha rasilimali kilimo Kigamboni ambako tuliwaita wakulima kujifunza mazao mbalimbali na jinsi ya kuweka dawa asili kuanzia katika kitalu mpaka kuhamishia shambani.

“Na sasa wale wakulima baada ya kutoka pale walitakiwa waje watekeleze kwenye mashamba yao na kufundisha wakulima wengine ambao hawakuja katika darasa lile. Pia AGENDA walitusaidia kusambaza miti ya matunda katika maeneo mbalimbali ambayo ni pamoja na shule za msingi na sekondari,”amesema Mhina

Wakati huo huo wanafuika wa mradi huo akiwemo mkulima Deocretus Rwamishale pamoja na Mwalimu wa taaluma Shule ya Msingi Rupia Winfrida Mwisaka wameishukuru AGENDA kwa kuwapatia mafunzo ya kilimo endelevu pamoja na kuwapatia miche ya miti ya matunda.



Na Seif Mangwangi, Michuzi TV Arusha

TANZANIA inaelezwa kuwa na utajiri wa miundombinu ya barabara wenye thamani ya zaidi ya Sh.trilioni 38 hivyo kazi kubwa ya Serikali ni kuhakikisha inalinda miundombinu hiyo kwa kuzifanyia ukarabati wa kila mara.

Hayo yameelezwa leo 9 Januari 2026, Jijini Arusha na Waziri wa Ujenzi Abdallah Ulega wakati wa ufunguzi wa mkutano wa chama cha mifuko ya matengenezo ya Barabara Afrika(ARMFA).

Aidha mkutano huo umetumika kumsimika Rais mpya wa chama hicho Mtanzania, Mhandisi Rashid kambanga ambaye ataongoza chama hicho kwa miaka miwili.

Ulega amesema chama hicho kimekuwa mhimili mkuu wa kuhakikisha barabara zinazotengenezwa zinatunzwa kwa kufanyiwa ukarabati wa mara kwa mara kwa kuwa zimekuwa zikitumika fedha nyingi kwenye ujenzi.

Amesema asilimia themanini ya usafiri nchini umekuwa ukitegemea miundo mbinu ya barabara hivyo ni jukumu la Serikali kuhakikisha kila wakati miundo mbinu hiyo inakuwa salama Ili kuendeleza shughuli za kiuchumi.

“ Hizi Barabara kuwa nazo ni jambo moja lakini kuzitunza ni jambo lingine, sasa hii bodi kazi yake kubwa ni pamoja na kuzitunza hizi barabara, na ndio sababu nchi za Afrika kupitia Kwa wataalam wake wakaamua kuuanda hiki chombo,” amesema.

Waziri Ulega amesema Tanzania na nchi sita zinazoizunguka ni wanufaikaji wakuu wa chama hicho kutokana na kuwa na matumizi makubwa ya barabara kutokana na uwepo wa bandari ambapo nchi hizo hupitisha mizigo yake.

“ Nchi za Jamhuri ya kidemokrasia ya Congo, Zambia, Malawi, Uganda, Burundi, Rwanda, zote zinategemea bandari yetu, uchumi wao inategemea barabara kwa kupitisha mizigo, Kwa hiyo ni muhimu sana kukarabati barabara,” amesema.

Rais mpya aliyekabidhiwa wadhifa huo ambaye pia ni Mtendaji Mkuu wa mfuko wa barabara nchini, Mhandisi Rashid Kambaga amesema mfuko wa barabara umekuwa na umuhimu mkubwa kwa kuwa unaisaidia Serikali kutunza miundombinu hiyo.

“ Serikali kwa kawaida ina mambo mengi sana, ukisema ijenge barabara na bado ikarabati itashindwa kutekeleza mambo mengine kwa hiyo mfuko huu unasaidia kutunza miundombinu hii katika nchi,” amesema.

Amesema umoja huo ni kuhakikisha wanashirikiana na wanabadilishana uzoefu wa namna ambavyo wamekuwa wakitekeleza jukumu la kutunza barabara katika nchi zao ikiwemo upatikanaji wa fedha.

“ Nchi nyingi huwa tunakosa rasilimali fedha kwaajili ya kukarabati barabara zetu, kwa hiyo huwa tunabadilishana uzoefu wa kujua wenzetu wamefanyaje lakini pia kujua chanzo kizuri cha kupata fedha na sisi tunaishauri Serikali zetu,” amesema.








Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Iringa, Daud Yassin, amewatembelea waandishi wa habari waliopata majeraha kufuatia ajali ya gari iliyotokea tarehe 5 Februari 2026 mkoani Iringa.

Ajali hiyo ilitokea katika Kijiji cha Idodi, Halmashauri ya Wilaya ya Iringa, wakati waandishi wa habari wakirejea kutoka Idodi walikohudhuria sherehe za maadhimisho ya miaka 49 ya kuzaliwa kwa CCM.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo hospitalini, Yassin amesema amefarijika kuona hali za afya za majeruhi hao zikizidi kuimarika siku hadi siku.

“Nimefarijika kufika tena hospitali kuwaona ndugu zangu wanahabari ambao walipata ajali hivi karibuni na kuona hali za afya zao zinazidi kuimarika. Tuna kila sababu ya kumshukuru Mungu kwa rehema hii ya uhai,” amesema Yassin.

Ameendelea kuwatakia waandishi hao uponaji wa haraka, huku akisisitiza mshikamano na mchango mkubwa wa wanahabari katika kuhabarisha jamii na kuunga mkono shughuli za maendeleo.

 

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi ametoa wito kwa sekta binafsi kushirikiana na Vyuo,kuwekeza katika tafiti hususan za sayansi na teknolojia ili kuinua viwango vya tafiti na ubora wa elimu nchini.

Makamu wa Rais amesema hayo wakati wa uzinduzi wa mpango waushirikiano kati ya Taasisi za Elimu na Waajiri, uliyofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) Jijini Dar es Salaam.

Amesema Kupitia Mpango huo, sekta binafsi inaweza kuchangia maendeleo ya elimu kwa kufadhili tafiti na kutoa ufadhili kwa wanafunzi wa fani mbalimbali kulingana na mahitaji ya soko la ajira.

Aidha, Makamu wa Rais ametoa wito kwa Taasisi za elimu na Sekta binafsi nchini kuzingatia maendeleo ya kasi ya sayansi na teknolojia duniani katika utekelezaji wa Mpango huo.

Amesema Vyuo na Sekta binafsi vishirikiane kubaini ujuzi muhimu unaohitajika sasa na siku zijazo hususan katika fani za sayansi, teknolojia, ubunifu, tiba, uhandisi na hesabu ili kuwezesha vijana kushindana na kupata nafasi katika soko la ajira nchini na kimataifa.

Makamu wa Rais amesema ushirikiano baina ya Taasisi za elimu na Viwandani hitaji la lazima katika dunia ya leo, kwa kuwa Vyuo haviwezi tena kuwavisiwa vya nadharia, na viwanda haviwezi kukua bila nguvukazi yenye ujuziunaoendana na teknolojia na ushindani wa soko.

Ameongeza kwamba, Serikali ya Awamu ya Sita imeweka kipaumbele chakimkakati katika kukuza ujuzi, stadi, maarifa na sifa za kuajirika au kujiajirimiongoni mwa vijana na wahitimu wa ngazi mbalimbali za elimu, ikitambuakwamba maendeleo endelevu ya Taifa hayawezekani bila kuwa narasilimaliwatu iliyoelimika na yenye uwezo wa kuchangia kikamilifu katikauchumi wa Taifa.

Amesema Serikali imeendelea kufanya maboresho makubwa ya sera namitaala ya elimu katika ngazi zote kwa lengo la kuujenga mfumo wa elimu uliomnyumbufu, jumuishi na unaoendana na vipaji, mwelekeo na mahitaji halisi ya soko la ajira, huku ikizingatia mabadiliko ya teknolojia na ushindani wakitaifa na kimataifa.

Uzinduzi wa Mpango huo ni utekelezaji wa ahadi ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan aliyoitoa wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu wamwaka 2025, ambapo aliahidi kuanzisha Mpango wa pamoja kati ya Waajiri, Vyuo vya ufundi stadi na Vyuo Vikuu kwa lengo la kulinganisha mafunzo namahitaji halisi ya sekta za kipaumbele za Taifa, ndani ya siku 100 baada ya kuapishwa kwake.

Pamoja na mambo mengine, Mpango wa ushirikiano kati ya Taasisi za Elimuna Viwanda unalenga kuimarisha uhusiano wa kimkakati kati ya utoaji waelimu na utendaji kazi, kwa lengo la kulinganisha mafunzo na mahitaji yasekta za kipaumbele kama nishati, Teknolojia ya Habari na Mawasiliano(TEHAMA) na viwanda vya kuongeza thamani.

Aidha, Mpango unawekamsingi thabiti wa kujenga kizazi cha wahitimu wenye uwezo wa kuajirika, kujiajiri na kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya Taifa kwani umedhamiriakubadilisha mfumo wa elimu ya nadharia kwenda mfumo unaozingatia ujuzi, vitendo, ubunifu na uzalishaji mali.

Uzinduzi huo, umehudhuriwa na Viongozi mbalimbali wa Serikali, Bunge, Dinipamoja na wadau wa maendeleo. Wengine waliohudhuria ni pamoja naWaajiri na Wamiliki wa Viwanda, Wakuu wa Taasisi mbalimbali, Wakuu waVyuo pamoja na Wanafunzi.

Kwa upande wake Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda, amesema kuwa uzinduzi wa Mpango wa Kitaifa wenye lengo la Kukuza Ujuzi na Ajira ni utekelezaji wa ahadi ya Rais Samia Suluhu Hassan aliyoitoa wakati wa Kampeni za uchaguzi kwa mwaka 2025 kwamba ndani ya siku 100 endapo atachaguliwa na kuapishwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Serikali ingeandaa na kuzindua Mpango wa kukuza ujuzi na uwezo wa kuajirika kwa vijana, na sasa ahadi hiyo imetimia kabla ya muda uliowekwa.

Prof. Mkenda ameeleza kuwa Mpango huu umeandaliwa kwa kushirikisha na wadau mbalimbali ikiwemo Vyuo vya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA), Waajiri na Wataalamu waliobobea katika kuboresha mitaala na kuongeza ujuzi akisisitiza kuwa ushirikiano huu ni msingi wa kuhakikisha Wahitimu wanapata ujuzi stahiki unaohitajika katika soko la ajira

"Yapo mafanikio tumeanza kuyaona ya ushirikino na viwanda, Wahitimu wa VETA, hususan VETA Moshi, wamekuwa wakipata ajira ndani na nje ya nchi katika maeneo kama Namibia, Guinea-Conakry, Mauritania, Kongo na Ghana hivyo uzinduzi huu utahamasisha waajiri kushirikiana zaidi, wazazi kuelewa umuhimu wa kuwapeleka watoto shuleni kupata ujuzi, na hatimaye kuchangia katika kuinua uchumi wa Tanzania," amesisitiza Prof Mkenda.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akizindua Mpango wa Ushirikiano kati ya Taasisi za Elimuna Viwanda katika hafla iliyofanyika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) Jijini Dar es Salaam, leo tarehe 09 Februari 2026.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akihutubia wakati wa Uzinduzi wa Mpango wa Ushirikiano kati ya Taasisi za Elimu na Viwanda uliyofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) Jijini Dar es Salaam, leo tarehe 09 Februari 2026.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, akiwa na Viongozi mbalimbali katika picha ya pamoja na baadhi ya Waajiri, mara baada ya kuzindua Mpango wa Ushirikiano kati ya Taasisi za Elimu na Viwanda katika hafla iliyofanyika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) Jijini Dar es Salaam, leo tarehe 09 Februari 2026.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akiwasili katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) Jijini Dar es Salaam kwaajili ya Uzinduzi wa Mpango waUshirikiano kati ya Taasisi za Elimu na Viwanda, leo tarehe 09 Februari 2026.



Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akiwa na Viongozi mbalimbali wakati akishiriki Uzinduzi waMpango wa Ushirikiano kati ya Taasisi za Elimu na Viwanda uliyofanyika katikaKituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) Jijini Dar es Salaam, leo tarehe 09 Februari 2026.


Serikali mkoani Geita imeikabidhi gari la zimamoto mamlaka ya mji mdogo wa Katoro gari ambapo linatarajiwa kuwa Msaada mkubwa kwa wananchi wa mji huo.

Mkuu wa mkoa wa Geita Martin Shigella amezindua gari hilo ambalo lina uwezo wa kubeba jumla ya Lita 5000 za maji ya kuzimia moto pamoja na form compound Lita 500.

Akizungumza na wananchi katika mji huo Shigela amewataka wananchi wa Katoro kulitumia na kulitunza vizuri gari hilo ambalo limekuja kuwa Msaada mkubwa ambapo hapo awali ilibidi kusafiri umbali mrefu kupata Msaada wa zimamoto.

Aidha Shigela ametoa maelekezo kwa mamlaka ya maji kuanzisha vituo vya maji sehemu mbalimbali katika mji huo ili gari hilo lisisafiri umbali mrefu kufata maji kwa ajili ya kuzimia moto.

"Mamlaka ya maji GEUWASA tuhakikishe tunaweka miondombinu ya maji Kila mahali ili vituo vya maji vipatikane Kila sehemu kwa ajili ya kuondoa usumbufu wa kujaza maji kwenye gari hili" alisema Shigela.

Kwa kipindi Cha mwaka 2025 mpaka 2026 mwanzoni jumla ya nyumba 10 na maduka 4 yalipata ajali ya moto ambapo gari ya kuzima moto huo ilikuwa ilikea Geita manispaa.

Jeshi la zimamoto mkoa wa Geita kimetoa wito kwa wananchi kutumia  namba ya dharula ya zimamoto kama ilivyoelekezwa na si kwa mambo binafsi.

Kaimu kamanda wa jeshi la zimamoto na  uoakoaji mkoa wa Geita ASF Kenneth Mwakasitu amesema kupitia namba 114 mwananchi atapata huduma ya zimamoto kwa masaa 24.

"Wananchi tujue matumizi sahihi ya namba hii ya dharula,hatutegemei matumizi mengine ya mzaha au michezo kwasbabu hii namba yetu ni kwa ajili ya kuzima moto na kufanya maokozi" alisema Mwakasitu

Nae mbunge wa Jimbo la Katoro Eng. Kija Ntemi amesema kuwa gari hili linaenda kuwapa ahueni wafanyabiashara katika mji huo ambao wamekuwa wakiishi kwa wasiwasi kutokana na ukosefu wa gari la zima moto katika maeneo ya karibu.








Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) imeibuka mshindi kwenye Tuzo za Kimataifa za Ujenzi Zanzibar (ZICA Awards) baada ya kutunukiwa tuzo ya Benki Bora katika Kuwezesha Miradi ya Ujenzi Zanzibar (Excellence in Financing Construction Projects in Zanzibar), hatua inayothibitisha mchango wake mkubwa katika kukuza sekta ya ujenzi visiwani humo.

Hafla ya utoaji wa tuzo hizo ilifanyika mwishoni mwa wiki visiwani Zanzibar, ikiongozwa na Mwenyekiti wa Chemba ya Taifa ya Biashara Zanzibar (ZNCC), Bw. Ali Suleiman Amour, na kuhudhuriwa na wadau mbalimbali wa sekta ya ujenzi kutoka serikalini na sekta binafsi. Benki ya NBC iliwakilishwa na Mkurugenzi wa Wateja Wakubwa na Uwekezaji, Bw. Elvis Ndunguru, aliyeongoza ujumbe wa maofisa wengine wa benki hiyo katika hafla hiyo.

Akizungumza mara baada ya kupokea tuzo hiyo, Bw. Ndunguru alisema ushindi huo ni muendelezo wa mafanikio na uthibitisho wa jitihada endelevu za NBC katika kuwezesha miradi ya ujenzi nchini - Tanzania Bara na Zanzibar. Alitaja miongoni mwa miradi mikubwa iliyofanikishwa kwa ushiriki wa benki hiyo visiwani humo kuwa ni ujenzi wa Kituo cha Abiria cha Vivuko cha Maruhubi (Mpiga Duru) kilichozinduliwa hivi karibuni, pamoja na ujenzi wa Kituo cha Afya cha Kizimkazi.

“Kwa upande wa Tanzania Bara, NBC imeendelea kuwa mstari wa mbele katika kuwezesha miradi mikubwa ya kimkakati ikiwemo miradi ya reli, madaraja na viwanja vya ndege. Tunatambua sekta ya ujenzi ni mhimili muhimu katika kukuza uchumi wa taifa, hivyo tutaendelea kushirikiana na serikali na sekta binafsi kuhakikisha miradi hiyo inafanikiwa, sambamba na kudhamini matukio muhimu ya wadau wa sekta hii,” alisema Bw. Ndunguru.

Benki ya NBC pia ilikuwa miongoni mwa wadhamini wakuu wa tuzo hizo za ZICA, ikionyesha dhamira yake ya dhati katika kuunga mkono maendeleo ya sekta ya ujenzi.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa ZNCC, Bw. Ali Suleiman Amour, aliwapongeza waandaaji wa tuzo hizo — CSW Group na Zanzibar Marketing — pamoja na washindi wote, akizitaja tuzo za ZICA kama jukwaa muhimu la kuhamasisha ubora, ushindani wa kitaaluma na uwajibikaji katika sekta ya ujenzi.

Kutokana na mchango mkubwa wa sekta ya ujenzi katika kuchochea maendeleo ya kiuchumi kupitia ukuaji wa miundombinu, biashara, utalii, makazi bora na uwekezaji, Bw. Amour aliziomba Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuimarisha ushirikiano zaidi, hususan katika kuweka sera na mazingira rafiki kwa wawekezaji wa sekta hiyo.

“Serikali pia ihakikishe inawajengea uwezo wazawa kupitia mafunzo, teknolojia na mitaji, sambamba na kusimamia viwango, ubora na ujenzi unaozingatia usalama na utunzaji wa mazingira. Kwa upande wa wadau wa sekta ya ujenzi, ni muhimu kuzingatia maadili, uwazi na sheria ili kujenga imani kwa jamii na serikali ambayo ndiyo mdau wao mkuu,” alisisitiza Bw. Amour.

Awali, akielezea mchakato wa utoaji wa tuzo hizo, Mkurugenzi wa Uendeshaji wa CSW Group, Bi. Annelise Nyangusi, aliwashukuru wadhamini wote wakiwemo Benki ya NBC, akibainisha kuwa vigezo vya kuwapata washindi vilijikita katika ubora wa huduma, ushirikiano wa soko pamoja na mbinu za kipekee za ufanisi wa kampuni.


Mwenyekiti wa Chemba ya Taifa ya Biashara Zanzibar (ZNCC), Bw. Ali Suleiman Amour (kushoto) akikabidhi tuzo ya Benki Bora katika Kuwezesha Miradi ya Ujenzi Zanzibar (Excellence in Financing Construction Projects in Zanzibar) kwa Mkurugenzi wa Wateja Wakubwa na Uwekezaji wa benki ya NBC Bw. Elvis Ndunguru baada ya benki hiyo kuibuka kinara wa tuzo hiyo kwenye Tuzo za Kimataifa za Ujenzi Zanzibar (ZICA Awards) zilizofanyika mwishoni mwa wiki Zanzibar. Wanaoshuhudia ni maofisa wengine wa benki hiyo.


Mwenyekiti wa Chemba ya Taifa ya Biashara Zanzibar (ZNCC), Bw. Ali Suleiman Amour (kushoto) akijadili jambo na Mkurugenzi wa Wateja Wakubwa na Uwekezaji wa benki ya NBC Bw. Elvis Ndunguru (kulia) wakati wa hafla ya Tuzo za Kimataifa za Ujenzi Zanzibar (ZICA Awards) zilizofanyika mwishoni mwa wiki Zanzibar. Benki ya NBC iliibuka kinara wa tuzo ya Benki Bora katika Kuwezesha Miradi ya Ujenzi Zanzibar (Excellence in Financing Construction Projects in Zanzibar).


Mwenyekiti wa Chemba ya Taifa ya Biashara Zanzibar (ZNCC), Bw. Ali Suleiman Amour (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na washindi mbalimbali wa tuzo Tuzo za Kimataifa za Ujenzi Zanzibar (ZICA Awards) zilizofanyika mwishoni mwa wiki Zanzibar. Kushoto ni Mkurugenzi wa Wateja Wakubwa na Uwekezaji wa benki ya NBC Bw. Elvis Ndunguru ambae benki yake iliibuka kinara wa tuzo ya Benki Bora katika Kuwezesha Miradi ya Ujenzi Zanzibar (Excellence in Financing Construction Projects in Zanzibar).





Mkurugenzi wa Wateja Wakubwa na Uwekezaji wa benki ya NBC Bw. Elvis Ndunguru (wa tatu kushoto) sambamba na maofisa wengine wa benki hiyo wakifurahia tuzo hiyo.


Jumla ya shilingi milioni 40 hukusanywa Kila mwezi kutoka kwa jumuiya za watoa huduma za maji ngazi ya jamii (CBWSO) katika wilaya ya Geita.

Hayo yamesemwa na meneja wa Wakala wa Maji na usafi wa mazingira vijijini RUWASA wilaya ya Geita  Injinia Sande Batakanwa katika mkutano wa nusu mwaka wa jumuiya za watoa huduma za maji ngazi ya jamii Yani CBWSO katika wilaya hiyo.

Batakanwa alisema kuwa kumekuwa na mafanikio makubwa tangu kuanzishwa kwa jumuiya hizo katika wilaya hiyo ambapo Sasa wananchi wanapata huduma Bora za maji ambazo zimefuikisha asilimia 60 ya upatikanaji wake katika wilaya ya Geita.

Lusekelo Mwaikenda afisa mtendaji kata ya Nyarugusu amekiri uwepo wa manufaa makubwa kupitia CBWSO hizi ambapo Sasa wananchi wanapata huduma za maji kwa wakati. 

Aidha aliongeza kuwa kufuatia kuwepo kwa mradi wa RUWASA katika kata ya Nyarugusu wananchi wameepukana na adha ya maji katika eneo Hilo ambapo hapo awali walitumi maji ya kwenye mabwawa ambayo si safi na salama.

Nae diwani wa kata ya Kaseme Andrew Kalamula alisema kuwa viongozi katika kata ya Kaseme wamekuwa wakihamasisha utunzajibwa mazingira ili kulinda na kuvitunza vyanzo vya maji na katika kata hiyo.








 

  

*Sekta ya mafuta na gesi kama nguzo ya maendeleo ya Taifa*

Na Rashid Mtagaluka.

Tarehe 14 Novemba 2025, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, aliwasilisha hotuba yake ya kwanza ya muhula mpya mbele ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, hotuba iliyobeba maelekezo ya kimkakati kuhusu mwelekeo wa Serikali katika kusimamia uchumi na rasilimali za Taifa.

Katika hotuba hiyo, Rais aliweka bayana dhamira ya Serikali ya kutumia ipasavyo rasilimali zilizopo, hususan mafuta na gesi asilia, kama chachu ya maendeleo ya viwanda, ukuaji wa uchumi na ustawi wa wananchi. Alisisitiza kuwa rasilimali hizo ni mhimili muhimu wa safari ya Taifa kuelekea maendeleo endelevu.

Ndani ya siku 100 za mwanzo wa muhula huo, sekta ya mafuta na gesi imeendelea kujitokeza kama moja ya nguzo kuu za utekelezaji wa dira hiyo, chini ya uangalizi wa Serikali kupitia Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC).

Tanzania ni miongoni mwa nchi zilizojaaliwa akiba kubwa ya gesi asilia, rasilimali ambayo ina uwezo mkubwa wa kubadili taswira ya uchumi wa Taifa endapo itasimamiwa kwa weledi, uwazi na uwajibikaji. 

Akihutubia Bunge, Rais Samia alisisitiza kuwa rasilimali hizi ni mali ya wananchi wote, hivyo matumizi yake lazima yaongozwe na maslahi ya Taifa kwa vizazi vya sasa na vijavyo.

Katika muktadha huo, TPDC imeendelea kutekeleza majukumu yake ya kisheria na kikatiba kama wakala wa Serikali katika sekta ya mafuta na gesi, kwa kuzingatia kikamilifu maelekezo na dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita.

Katika siku 100 za mwanzo wa muhula mpya wa Rais Samia, juhudi zimeelekezwa katika kuimarisha usimamizi wa rasilimali za gesi asilia, kusimamia mikataba ya utafutaji na uzalishaji, kuimarisha ushirikiano na wawekezaji, pamoja na kuhakikisha kuwa rasilimali hii inaleta manufaa ya moja kwa moja kwa wananchi.

Moja ya maeneo yaliyopata uzito mkubwa katika hotuba ya Rais ni matumizi ya gesi asilia kama nishati safi, nafuu na salama kwa ajili ya viwanda, uzalishaji wa umeme na matumizi ya majumbani. 

Ndani ya kipindi hiki cha siku 100, Serikali kupitia taasisi zake ikiwemo TPDC, imeendelea kusimamia na kuimarisha miradi ya uzalishaji na usambazaji wa gesi asilia katika maeneo mbalimbali ya nchi.

Hatua hizi zinalenga kupunguza gharama za uzalishaji viwandani, kukuza uchumi wa ndani na kuongeza fursa za ajira kwa Watanzania, sambamba na kupunguza utegemezi wa nishati zisizo rafiki kwa mazingira.

Aidha, Rais Samia alisisitiza umuhimu wa sekta ya mafuta na gesi kuchangia maendeleo ya jamii zinazozunguka maeneo ya uzalishaji. Katika siku 100 hizi, dhana ya Uwajibikaji wa Kampuni kwa Jamii (CSR) imeendelea kupewa kipaumbele katika utekelezaji wa majukumu ya TPDC.

Kupitia miradi ya kijamii katika sekta za elimu, afya, maji na miundombinu, juhudi zimeelekezwa katika kuhakikisha kuwa wananchi wanapata manufaa ya moja kwa moja ya uwepo wa rasilimali hizi katika maeneo yao.

Katika hotuba yake, Rais Samia aligusia pia umuhimu wa kujenga uwezo wa Watanzania kushiriki kikamilifu katika sekta ya mafuta na gesi. Ndani ya siku 100, jitihada zimeendelea kuimarisha ushiriki wa wazawa (local content) kwa kutoa fursa kwa wataalamu wa ndani, makampuni ya Kitanzania na vijana wanaosomea masuala ya nishati.

Hatua hii inaakisi dhamira ya Serikali ya kuhakikisha kuwa sekta ya mafuta na gesi haiwanufaishi wawekezaji pekee, bali inakuwa jukwaa la kukuza ajira, ujuzi na teknolojia kwa Watanzania.

Sambamba na hilo, masuala ya ulinzi wa mazingira na usalama yameendelea kupewa uzito unaostahili. 

Akihutubia Bunge, Rais Samia alisisitiza kuwa maendeleo ya kiuchumi hayawezi kupatikana kwa gharama ya mazingira. Ndani ya siku 100, TPDC imeendelea kusimamia shughuli za utafutaji, uzalishaji na usambazaji wa gesi kwa kuzingatia viwango vya kitaifa na kimataifa vya uhifadhi wa mazingira, afya na usalama kazini.

Kwa ujumla, siku 100 za mwanzo wa muhula mpya wa Rais Samia Suluhu Hassan zimeonesha mwelekeo thabiti wa Serikali katika kusimamia sekta ya mafuta na gesi kwa maslahi mapana ya Taifa. 

Kupitia TPDC, Serikali imeendelea kuimarisha misingi ya usimamizi bora wa rasilimali, kuongeza uwazi na kuimarisha mchango wa sekta hii katika uchumi wa Taifa.

Ingawa safari ya maendeleo ya sekta ya mafuta na gesi bado ni ndefu na yenye changamoto, dalili zilizojitokeza ndani ya siku 100 hizi zinaonesha dhamira ya dhati ya Serikali ya Awamu ya Sita kuhakikisha kuwa rasilimali hii inakuwa baraka kwa Watanzania wote.

Katika kutekeleza maono aliyoyatoa bungeni tarehe 14 Novemba 2025, Rais Samia ameendelea kusisitiza mshikamano kati ya Serikali, taasisi zake, sekta binafsi na wananchi. Sekta ya mafuta na gesi, chini ya usimamizi wa TPDC, inaendelea kubaki kuwa moja ya nguzo muhimu katika safari ya Tanzania kuelekea uchumi wa kati wa juu na maendeleo jumuishi. Siku 100 hizi ni mwanzo tu, lakini ni mwanzo unaobeba matumaini makubwa kwa mustakabali wa Taifa.




SERIKALI imezidisha kasi ya kujenga uchumi wa kidijitali kwa kusisitiza matumizi mapana ya mfumo wa anwani za makazi, hatua inayolenga kurahisisha utoaji wa huduma, kuimarisha utambuzi wa wananchi na kuongeza ufanisi wa shughuli za kiuchumi nchini. Wito huo umetolewa na Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Angella Kairuki, akizihimiza wizara na taasisi zote za umma kuutumia kikamilifu mfumo huo kama nyenzo muhimu ya maendeleo ya kisasa.

Akizungumza jijini Dar Es Salaam leo Januari 08, 2026 katika kilele cha Wiki ya Anwani za Makazi na Maonyesho ya Teknolojia ya Posta jijini Dar es Salaam, Kairuki ameeleza kuwa mfumo huo ni mhimili wa kutambua makazi ya wananchi, kurahisisha huduma za kijamii na kiuchumi pamoja na kuboresha ukusanyaji wa mapato ya serikali. Hafla hiyo ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa kitaifa wakiwemo Hassan Juma, Anne Semamba Makinda na Profesa Joyce Mzalishako.

Waziri Kairuki amebainisha kuwa serikali imeendelea kuwekeza katika miundombinu ya mawasiliano na mifumo ya kidijitali ili kuiwezesha Tanzania kufikia uchumi unaotegemea ubunifu, teknolojia na maarifa. Alisema hadi sasa anwani za makazi takribani milioni 12.9 zimeshasajiliwa, huku mifumo 29 kutoka taasisi 23 za umma na binafsi ikiunganishwa ili kuboresha utoaji wa huduma.

Ameeleza kuwa manufaa ya mfumo huo yameonekana katika sekta za elimu, fedha, usalama, biashara mtandao na huduma za dharura, ambapo taasisi kama Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu na Jeshi la Zimamoto zimeongeza ufanisi wa utekelezaji wa majukumu yao. Pia mfumo umeisaidia serikali kufikisha misaada kwa haraka wakati wa majanga kwa kutambua kaya zilizoathirika.

Kwa upande wa ushiriki wa sekta binafsi, Kairuki amezihimiza benki, kampuni za mawasiliano na taasisi za fedha kuutumia mfumo wa anwani za makazi katika utambuzi wa wateja, hatua itakayorahisisha huduma za kifedha na kuongeza ujumuishi wa wananchi katika uchumi rasmi. Sambamba na hilo, wizara ilikabidhi zaidi ya vishikwambi 5,000 kwa watendaji wa mitaa, kata na vijiji ili kuharakisha uingizaji na usasishaji wa taarifa za makazi.

Aidha, ameipongeza TAMISEMI, Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar na Wizara ya Ardhi kwa ushirikiano uliofanikisha utekelezaji wa mradi huo kwa muda mfupi. Amesisitiza kuwa Wiki ya Anwani za Makazi itaadhimishwa kila Februari 8 kama jukwaa la tathmini, ubadilishanaji uzoefu na uhamasishaji wa matumizi ya teknolojia katika huduma za posta na mawasiliano.

Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Mohammed Hamisa Abdullah, amesema mfumo wa anwani za makazi ni sehemu ya mkakati wa kitaifa wa kuimarisha utambuzi wa makazi na kurahisisha huduma za serikali na sekta binafsi. Aliongeza kuwa mfumo huo uliobuniwa na wataalamu wa ndani unapatikana kupitia tovuti na programu ya simu ya NAPA, huku idadi ya watumiaji ikiongezeka kwa zaidi ya asilimia 70 ikilinganishwa na mwaka uliopita.

Naye Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar, Hassan Juma, amesisitiza dhamira ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuendeleza ushirikiano katika utekelezaji wa mfumo huo Unguja na Pemba. Alisema licha ya changamoto za awali za uelewa mdogo, elimu kwa umma na ushiriki wa viongozi wa mitaa umeongeza matumizi ya huduma za kidijitali, zikiwemo mikopo ya elimu, huduma za benki na utambuzi sahihi wa makazi.









Top News