

Na Janeth Raphael MichuziTv
Maonesho ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba) yameelezwa kuwa moja ya majukwaa makubwa yanayochochea ukuaji wa biashara, uwekezaji na ubunifu nchini, huku yakiiunganisha Tanzania na masoko ya kikanda pamoja na ya kimataifa.
Akizungumza katika ufunguzi rasmi Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam leo, Ijumaa Julai 3, 2026, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema maonesho hayo yameendelea kuwa nguzo muhimu ya maendeleo ya sekta ya biashara kwa kipindi cha nusu karne.
Rais Samia amesema Sabasaba imekuwa jukwaa linalowakutanisha wazalishaji, wafanyabiashara, wawekezaji na wanunuzi kutoka ndani na nje ya nchi, jambo ambalo limeongeza fursa za biashara na kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi.
Amebainisha kuwa mafanikio ya maonesho hayo yanaonekana kupitia wafanyabiashara wengi walioanza safari zao kwa mitaji midogo wakitumia Sabasaba kutangaza bidhaa na huduma zao, lakini sasa wamekua na kuwa miongoni mwa wafanyabiashara wakubwa wanaochangia kwa kiasi kikubwa ukuaji wa uchumi wa taifa.
Aidha, amesema maonesho hayo yameendelea kuwa chanzo cha manufaa kwa wakulima, wajasiriamali na wabunifu kwa kuwapatia nafasi ya kutafuta masoko mapya, kujifunza teknolojia na mbinu za kisasa za uzalishaji, pamoja na kupata washirika na mitaji ya kukuza shughuli zao za kiuchumi.
Kwa mujibu wa Rais Samia, Sabasaba imeendelea kuijengea Tanzania taswira nzuri kama kitovu cha biashara na uwekezaji katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kusini mwa Afrika, huku pia ikifungua milango ya masoko katika Bara la Afrika na sehemu nyingine duniani.
Ametoa wito kwa waandaaji wa maonesho hayo pamoja na wadau wa sekta binafsi kuendelea kubuni mbinu mpya zitakazoyawezesha Maonesho ya Sabasaba kufikia viwango vya kimataifa, ili yaendelee kuwa chachu ya ukuaji wa uchumi, ajira na maendeleo ya biashara nchini.


Tanzania ipo tayari kwa mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON 2027) ikiwa mwenyeji kwa kushirikiana na Kenya na Uganda ambapo maandalizi yamefikia hatua nzuri kwa kuzingatia viwango vya Shirikisho la Mpira wa Miguu Barani Afrika (CAF) vinavyotakiwa.
Akizungumza hii leo Julai 3, 2026 Jijini Arusha kwa niaba ya Mwenyekiti wa Kamati ya Kitaifa ya Makatibu Wakuu ya Maandalizi ya Michuano hiyo, Dkt. Jim Yonazi, Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii Dkt. Hassan Abbasi amesema Serikali imejipanga kikamilifu kuhakikisha michuano hiyo inafana kwa kuzingatia mipango na mikakati thabiti iliyopo.
Dkt. Abbasi ameiongoza Kamati hiyo iliyotembelea viwanja vitakavyotumika wakati wa michuano hiyo ikiwemo Kiwanja cha Mazoezi cha Mgambo, kiwanja cha mazoezi cha Engutoto, Kiwanja cha mazoezi Magereza, uwanja Mpya wa Arusha pamoja na ukaguzi wa barabara za mjini zinazosimamiwa na Wakala wa Barabara Tanzania-TANROADS pamoja na zinasosimamiwa na Wakala wa Barabara za mjini na vijijni -TARURA zitakazoingia na Kutoka Katika uwanja wa Arusha, kujionea maendeleo ya ukarabati na maboresho mbalimbali kuelekea michuano hiyo.
Aidha amesema kuwa, michuano hiyo itakuwa ya kihistoria kwa kukutanisha na kuvutia mamilioni ya watu barani Afrika na duniani kote, ambapo ni kwa mara ya kwanza mashindano hayo kuandaliwa kwa pamoja na Mataifa matatu ya Afrika Mashariki.
Aliongezea kuwa, Tanzania imejipanga kupokea Maelfu ya mashabiki, wachezaji, na viongozi wa soka wanatarajiwa kukusanyika na kuleta mwamko mkubwa kupitia Mashindano Makubwa ya Kombe la Mataifa Afrika (AFCON 2027).
"Ni wakati wetu sasa, kuipa nchi heshima yake kuelekea Michuano hiyo ya AFCON, kila mmoja akae tayari katika eneo lake na kujua kuwa anajukumu la kuifanikisha michuano hii na kwa viwango vya kimataifa," alisema Dkt. Abbasi.
Pia alisisistiza Wakandarasi kwenye miradi mbalimbali ya kuboresha miundombinu kuongeza kasi ili kumaliza kazi hizo kwa wakati bila kukwamisha maandalizi hayo.
Kwa upande wake Katibu Tawala wa Mkoa wa Arusha Dkt. Toba Nguvila amesema kuwa mkoa umeendelea na maandalizi yote muhimu ikiwemo ya ukarabati wa miundombinu itakayotumika, kuhakikisha upatikanaji wa huduma za maji, kuboresha maeneo ya utoaji wa huduma za kiafya ikiwemo hospitali, masuala ya mawasiliano, pamoja na umeme na kuhakikisha vinapatikana kwa ubora na viwango.
“Jiji linaimarisha miundombinu ya barabara, huku kukiwa na ujenzi na ukarabati wa hoteli za kutosha zitakazotoa huduma pamoja na uboreshwaji wa vituo vya afya vya kutolea huduma za afya ikiwemo hospitali ya Mount Meru, JKCI pamoja na NSK ambazo zitatoa huduma za kiafya kwa ubora na viwango,” alisema Dkt. Nguvila.




































.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)


.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)
