Na Janeth Raphael MichuziTv - Bungeni Dodoma 

Serikali imechukua Hatua Kudhibiti Migogoro ya Wakulima na Wafugaji Mto Lukuledi Ndanda

Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI imesema inatambua changamoto ya uvamizi wa wafugaji katika maeneo ya wakulima katika ushoroba wa Mto Lukuledi, Jimbo la Ndanda, hususan wakati wa ukame ambapo migogoro ya matumizi ya ardhi huongezeka.

Akijibu swali bungeni leo Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI) Dkt  Jafar Seif ameeleza kuwa Serikali kwa kushirikiana na Mamlaka za Serikali za Mitaa pamoja na vyombo vya ulinzi na usalama imekuwa ikichukua hatua mbalimbali za kudhibiti hali hiyo ili kuhakikisha amani na utulivu vinadumishwa kati ya wakulima na wafugaji.

Serikali imeeleza kuwa moja ya hatua kubwa zilizochukuliwa ni pamoja na kupima na kutenga maeneo maalum ya malisho yenye ukubwa wa takribani hekta 129,489.48 katika vijiji 30 vya Mkoa wa Lindi, ikiwemo vijiji vilivyo karibu na bonde la Mto Lukuledi, Ndanda. Hatua hii inalenga kupunguza msongamano wa mifugo katika maeneo ya kilimo na kuzuia migogoro inayojitokeza mara kwa mara.

Aidha, Serikali inaendelea kutoa elimu kwa wafugaji kuhusu umuhimu wa kuachana na ufugaji wa kuhamahama na badala yake kuelekea katika ufugaji wa kisasa unaozingatia tija na biashara. Elimu hiyo inalenga pia kubadilisha mtazamo kuhusu matumizi bora ya ardhi na uhifadhi wa mazingira.

Serikali imetoa wito kwa wafugaji kote nchini kuhakikisha wanazingatia mipango ya matumizi bora ya ardhi pamoja na kutumia kikamilifu maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya malisho kwa kuyaendeleza kupitia kuondoa vichaka na kupanda malisho yanayoendana na ikolojia ya maeneo husika.

Kwa mujibu wa Serikali, utekelezaji wa mikakati hiyo utasaidia kuhakikisha upatikanaji wa malisho ya kutosha mwaka mzima, kupunguza migogoro ya mara kwa mara kati ya wakulima na wafugaji, na hatimaye kuimarisha amani na maendeleo endelevu katika maeneo ya vijijini.



NA DENIS MLOWE IRINGA


ZAIDI ya vijana 200 kutoka vijiji 61 vinavyozunguka Shamba la Miti la Taifa la Sao Hill wilayani Mufindi, mkoani Iringa, wamehitimu mafunzo maalumu ya kukabiliana na majanga ya moto wa misitu ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha ulinzi wa rasilimali za misitu na mazingira kwa ujumla.

Mafunzo hayo yametolewa baada ya kufanyika mchakato wa usaili uliowahusisha zaidi ya vijana 400 waliojitokeza kupima utimamu wa mwili na akili kwa lengo la kushiriki katika kikosi cha kukabiliana na moto wa misitu hatua hiyo imeelezwa kuwa ni mkakati wa kuhakikisha kunakuwa na nguvu kazi ya kutosha yenye uelewa wa masuala ya usalama wa misitu katika maeneo yanayozunguka shamba hilo kubwa la miti.

Akizungumza wakati wa zoezi hilo, Msaidizi wa Mhifadhi Mkuu wa Shamba la Miti la Taifa la Sao Hill, PCO Said Singano, alisema ushirikishwaji wa vijana kutoka vijiji vinavyozunguka shamba hilo ni njia bora ya kujenga uelewa wa pamoja kuhusu umuhimu wa kulinda misitu na kuzuia hasara zinazoweza kusababishwa na moto.

Alisema moto wa misitu umekuwa tishio kubwa katika maeneo mbalimbali ya misitu nchini, hivyo ni muhimu kuendelea kutoa elimu na mafunzo kwa wananchi wanaoishi karibu na maeneo hayo ili wawe sehemu ya suluhisho la changamoto hiyo.
Aliongeza kuwa vijana waliopatiwa mafunzo wamefundishwa mbinu mbalimbali za kutambua vihatarishi vya moto, namna ya kuzuia kuenea kwa moto pamoja na hatua za haraka za kuchukua pindi moto unapozuka.

Singano alisema kuwa ushiriki wa wananchi katika shughuli za uhifadhi umeendelea kuleta matokeo chanya kwa kuwa jamii imekuwa na uelewa mkubwa zaidi kuhusu thamani ya misitu katika maendeleo ya kiuchumi na uhifadhi wa mazingira.

Alibainisha kuwa Shamba la Miti la Taifa la Sao Hill linaendelea kushirikiana na vijiji vinavyolizunguka ili kuhakikisha misitu inalindwa kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Kwa upande wake, Afisa wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Wilaya ya Mufindi, Sajenti Guntramu Mlenge, alisema ushirikiano uliopo kati ya Jeshi la Zimamoto na Uokoaji pamoja na Shamba la Miti la Sao Hill umechangia kwa kiasi kikubwa kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu namna ya kujikinga na majanga ya moto.

Alisema kupitia mafunzo hayo, vijana wamepata maarifa ya kutumia vifaa vya kuzimia moto, kutengeneza njia za kuzuia moto kuenea pamoja na mbinu za kufanya doria katika maeneo yenye hatari kubwa ya kutokea kwa moto. A

Aidha, alieleza kuwa elimu hiyo itawasaidia vijana kuwa mabalozi wa usalama wa mazingira katika vijiji vyao.

Baadhi ya vijana walioshiriki mafunzo hayo wameeleza kufurahishwa na fursa waliyoipata wakisema kuwa imewaongezea ujuzi na kuwapa nafasi ya kushiriki moja kwa moja katika shughuli za kulinda misitu.

Walisema maarifa waliyojifunza yatawasaidia kutoa elimu kwa wananchi wengine kuhusu madhara ya moto wa misitu na umuhimu wa kuhifadhi mazingira.

Hatua ya kuwajengea uwezo vijana katika maeneo yanayozunguka Shamba la Miti la Taifa la Sao Hill inaonekana kuwa sehemu muhimu ya mkakati wa kupunguza matukio ya moto wa misitu ambayo yamekuwa yakisababisha hasara kubwa kwa mazingira, uchumi na maendeleo ya jamii.

Serikali na wadau wa uhifadhi wanaamini kuwa ushiriki wa wananchi, hususan vijana, ni nguzo muhimu katika kuhakikisha misitu inalindwa na kuendelea kuwa rasilimali yenye manufaa kwa taifa.









Na Janeth Raphael - MichuziTv 

Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) umeendelea kuwa chachu ya mabadiliko kwa kaya maskini, hususan wanawake, kwa kuwawezesha kujikwamua kiuchumi na kuanza maisha ya kujitegemea.

Akizungumza katika kilele cha Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma jijini Dodoma, Kaimu Mkurugenzi wa Ukaguzi wa Ndani wa TASAF, aliyemwakilisha Mkurugenzi Mtendaji wa TASAF, Bw. Uswege Edward, amesema taasisi hiyo imewashirikisha baadhi ya wanufaika wa mpango katika banda la maonesho ili kuonesha mafanikio yaliyopatikana kupitia utekelezaji wa TASAF Awamu ya Pili.

Amesema wanufaika hao kutoka Tanzania Bara na Visiwani wameweza kunufaika kwa njia mbalimbali, ikiwemo kupata mitaji, vifaa vya uzalishaji na fursa zilizowasaidia kuanzisha au kuendeleza shughuli za kiuchumi zinazowaingizia kipato.

"Tunajivunia mafanikio ya walengwa wetu maana wakati wa usajili baadhi yao walikuwa wakikabiliwa na changamoto kubwa za maisha, ikiwemo kushindwa kumudu milo mitatu kwa siku. Leo hii wengi wao wanaendesha biashara na shughuli mbalimbali za kiuchumi zinazowapa kipato na kuwafanya wajitegemee", amesema Uswege.

Aidha, amesema TASAF inaamini imefanikiwa kuwasaidia walengwa wengi kuondokana na utegemezi na kuanza safari ya kujitegemea kiuchumi.

Kwa upande wake, mmoja wa wanufaika wa mpango huo, Devota Karia, ameishukuru TASAF kwa kuwapatia nafasi ya kushiriki katika maadhimisho hayo, akieleza kuwa yamekuwa fursa muhimu ya kutangaza biashara zao na kupata wateja wapya.

Pia amemshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuunga mkono na kuimarisha utekelezaji wa mpango wa TASAF, ambao umeleta matumaini mapya kwa maelfu ya kaya nchini.




 

Na Janeth Raphael MichuziTv - Bungeni Dodoma

Serikali imeeleza mpango wake wa kuimarisha sekta ya korosho nchini kwa kuongeza uwekezaji katika ubanguaji na uchakataji wa zao hilo, lengo likiwa ni kuhakikisha Tanzania inanufaika zaidi kupitia ongezeko la thamani ya mazao yake.

Akijibu swali bungeni Leo, Naibu Waziri wa Kilimo David Silinde lililoulizwa na Abdallah Dadi Chikota kuhusu vivutio kwa wabanguaji wa korosho wa ndani, Serikali imesema inaendelea kuboresha mazingira ya uwekezaji ili kuvutia zaidi viwanda vya kuchakata korosho ndani ya nchi.

Silinde amesema hatua mbalimbali zimechukuliwa, ikiwemo ujenzi wa Kongani ya Viwanda ya Maranje ambayo imewekewa miundombinu muhimu kama barabara, umeme na maji ili kurahisisha shughuli za uzalishaji na uwekezaji.

Aidha, kongani hiyo imesajiliwa kupitia TISEZA, hatua inayowapa wawekezaji fursa ya kupata vivutio mbalimbali vya kiuwekezaji vinavyotolewa na Serikali.

Serikali imesisitiza kuwa itaendelea kuimarisha mazingira ya sekta ya korosho ili kuongeza kiwango cha ubanguaji ndani ya nchi. Lengo kuu ni kuhakikisha ifikapo mwaka 2030, sehemu kubwa ya korosho zinazozalishwa nchini zinachakatwa hapa nchini, sambamba na kufikia uzalishaji wa hadi tani 1,000,000 kwa mwaka.

Hatua hiyo inalenga kuongeza thamani ya mazao ya ndani, kuimarisha ajira na kuongeza ushindani wa Tanzania katika soko la dunia linalozidi kuhitaji bidhaa zilizopewa thamani zaidi badala ya malighafi.


Na Mwandishi Wetu.

WAKALA wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA) umezidi kujipambanua kama muhimili na nguzo madhubuti katika kuchochea ukuaji wa uchumi wa taifa, kupitia mikakati yake endelevu inayolenga kurasimisha shughuli za kiuchumi na kuhakikisha hakuna Mtanzania anayeachwa nyuma katika upatikanaji wa huduma za sajili na leseni.

Hayo yamebainishwa na Ofisa Mtendaji Mkuu wa BRELA, Godfrey Nyaisa, alipokuwa akifungua kikao kazi cha wafanyakazi wa Wakala hiyo kilichofanyika mkoani Morogoro ambapo ametumia nafasi hiyo kuelezea kwa kina mafanikio ya wakala huo katika kuendelea kuwahudumia Watanzania.

“Katika mwaka wa fedha wa 2025/2026, BRELA imefanikiwa kuvuka malengo na kutekeleza majukumu yake ya msingi kwa ufanisi mkubwa ikijikita katika kuboresha huduma kwa wadau, kuimarisha mifumo ya kidijitali, kupanua wigo wa urasimishaji biashara nchini licha ya changamoto za kimazingira na kiuchumi zilizojitokeza” amesema Nyaisa

Kwa upande wake Kaimu Meneja wa Sehemu ya Mipango, Utafiti na Ubunifu wa BRELA Alinda Lema, amebainisha mafanikio hayo yamepatikana kupitia usimamizi thabiti wa Mpango Mkakati wa miaka mitano wa 2021/22–2025/26.

Amefafanua katika kipindi cha kuanzia Julai 2025 hadi Juni 2026, mpango huo umewezesha mazingira ya biashara nchini kwa kuimarisha huduma za sajili na leseni, mifumo ya kiteknolojia, na usimamizi wa utendaji kazi wa watumishi.

Pia kumekuwa na ongezeko la kasi ya urasimishaji wa biashara, kuimarika kwa ulinzi wa haki miliki, na kurahisishwa kwa huduma zote zinazowafikia wadau wa sekta binafsi na ya umma.

“Kampuni zilizosajiliwa nchini zilipanda kutoka 18,541 katika mwaka wa fedha uliopita wa 2024/25 na kufikia kampuni 19,264 katika mwaka wa fedha wa 2025/26, ikiwa ni ongezeko la asilimia 4 linaloakisi kuongezeka kwa imani ya wawekezaji wa ndani na nje.

“Katika urasimishaji wa biashara, usajili wa majina ya biashara uliongezeka kutoka majina 31,123 hadi kufikia 35,362, ikiwa ni ongezeko la asilimia 14,”amesema Lema.

Kwa upande wa sekta ya viwanda na miliki ubunifu nayo haikuachwa nyuma, kwani ilionyesha ukuaji unaochochea azma ya Tanzania kuwa nchi ya viwanda na uchumi wa kati.

Lema ameeleza kuwa utoaji wa leseni za viwanda uliongezeka kwa asilimia 50, kutoka leseni 435 hadi leseni 651 katika kipindi cha mwaka mmoja tu.

Pia utoaji wa Hataza kwa ajili ya kulinda wavumbuzi wa ndani ulishuhudia mapinduzi kwa kuongezeka kutoka hataza 30 hadi 61, ambalo ni ongezeko la asilimia 103, wakati usajili wa alama za biashara na huduma (Trade and Service marks) ukiongezeka kwa asilimia 10 kutoka sajili 3,148 hadi kufikia 3,455, hatua inayolinda alama na ubunifu wa wafanyabiashara sokoni.

BRELA ilitekeleza zoezi la kaguzi elimishi kwa upande wa leseni katika soko kuu la kimkakati la Kariakoo jijini Dar es Salaam. Ukaguzi huo haukulenga kuadhibu, bali kuweka mazingira rafiki ya uendeshaji biashara na uwekezaji kwa kutoa elimu ya uzingatiaji wa sheria za nchi.

Kuhusu uwazi na udhibiti wa mifumo ya kifedha, Wakala huo ulifanikiwa kufanya ukaguzi wa kina wa taarifa za wamiliki manufaa katika mkoa wa Arusha, hatua iliyosaidia kuongeza uelewa na kupunguza makosa yaliyokuwa yanajitokeza katika mfumo wa usajili wa kampuni.

Mkakati huu wa ukaguzi ulienda sambamba na utoaji endelevu wa elimu kwa umma kuanzia Julai 2025 hadi Juni 2026, ambapo BRELA ilitumia mbinu mbalimbali za kisasa kuwafikia wananchi.



Dodoma

Katibu Tawala wa Mkoa wa Arusha, Dkt. Toba Nguvila, amepongeza matumizi ya mfumo wa kisasa wa Supervisory Control and Data Acquisition (SCADA) unaotumiwa na Wakala wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (PBPA), akisema umeongeza uwazi na ufanisi katika usimamizi wa mafuta nchini.

Dkt. Nguvila alitoa pongezi hizo Juni 23, 2026, alipotembelea banda la PBPA katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali jijini Dodoma na kupata maelezo kuhusu namna mfumo huo unavyofanya kazi.

Alisema matumizi ya teknolojia za kisasa katika sekta ya mafuta yanaisaidia Serikali kufuatilia kwa karibu mwenendo wa mafuta yanayoingia nchini na kuhifadhiwa katika maghala mbalimbali, hivyo kudhibiti upotevu na kuongeza uwajibikaji.

“Ni jambo la kutia moyo kuona taasisi za umma zinatumia teknolojia za kisasa katika kuboresha usimamizi wa rasilimali za taifa. Mfumo huu unasaidia kuongeza uwazi na kuhakikisha mafuta yanayopokelewa yanafika katika maeneo yaliyokusudiwa,” alisema Dkt. Nguvila.

Akitoa maelezo kwa mgeni huyo, Mkaguzi wa Mafuta wa PBPA, Bw. Issa Khamis Mwitazy, alisema mfumo wa SCADA umechangia kwa kiasi kikubwa kudhibiti upotevu wa mafuta ambao kwa muda mrefu ulikuwa changamoto katika sekta hiyo.

Bw. Mwitazy alisema mfumo huo hulinganisha kiwango cha mafuta kilichopokelewa kutoka melini na kiwango kilichofika kwenye maghala, ambapo taarifa hutolewa mara moja endapo kutabainika tofauti yoyote ili hatua za haraka zichukuliwe.

Aidha, alisema mfumo huo unasoma na kufuatilia kwa wakati halisi ujazo wa mafuta kupitia mita za Serikali zilizopo katika bandari za Dar es Salaam, Tanga na Mtwara, pamoja na kusoma kiwango cha mafuta kilichopo katika maghala ya kampuni za mafuta.

Kwa mujibu wa PBPA, matumizi ya mfumo wa SCADA ni sehemu ya jitihada za Serikali za kuimarisha usimamizi wa mafuta nchini na kuhakikisha sekta hiyo inaendeshwa kwa uwazi, ufanisi na tija zaidi.


NA: DK. REUBENI LUMBAGALA

Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ni chombo muhimu nchini katika kuhakikisha mipango na mikakati ya maendeleo inatimizwa kikamilifu. Hii inatokana na ukweli kuwa mipango mingi ya maendeleo kama uboreshaji wa sekta za elimu, afya, maji, masoko, viwanda, umeme, barabara, makazi, biashara, inategemea upatikanaji wa raslimalifedha ili ziwezeshe utekelezaji wake.

TRA ina wajibu wa kukusanya kodi kutoka kwa walipakodi wake kama wafanyabiashara, wawekezaji, wafanyakazi na wajasiriamali mbalimbali. Mafanikio ya ukusanyaji kodi, ndiyo msingi wa kuiwezesha serikali kutimiza mipango yake ya maendeleo kwa ustawi na maendeleo ya wananchi.

Sasa TRA imetimiza miaka 30 tangu kuanzishwa kwake. TRA imepata mafanikio makubwa sana hasa katika uongozi wa serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan.

Rais Dk. Samia aliweka msingi wa serikali yake mapema kwa kuiagiza TRA iwajibike ipasavyo katika kukusanya mapato, lakini mapato hayo yasiwe ya dhuluma. Rais Dk. Samia anataka kila mwananchi mwenye sifa za kulipa kodi alipe.

Aprili 6, 2021, Rais Dk. Samia alipokuwa akiwaapisha makatibu wakuu na manaibu wao, alitoa maelekezo mahsusi kwa TRA. "Kukusanya kodi kwa mabavu havisaidii kwa muda mrefu. Nimepewa takwimu ya zile taskforce (vikosikazi vya kukusanya kodi) mlizoziunda lakini havisaidii, mnawatisha watu wanalazimika kufunga biashara."

"Tunazitaka kodi lakini kodi za dhuluma hapana. Kwa sababu hazitatufikisha mbali. Jinsi ya kurudisha wafanyabiashara, kutengeneza wigo wa kukusanya kodi, nafahamu uamuzi huu niliochukua tutayumba kwa miezi miwili, mitatu lakini baada ya muda tutarudi vizuri," amesema Rais Dk. Samia.

Msisitizo wa kuongeza mapato ulitokana na ukweli kuwa mipango mingi na mizuri aliyonayo Rais Dk. Samia kwa wananchi wake, haitaweza kufanikiwa kama TRA haitakusanya kodi kikamilifu ambayo ndiyo kichochea cha kufanikisha utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Awali, TRA ilikuwa na utaratibu wa kufunga biashara na shughuli mbalimbali pale ambapo mlipakodi atashindwa kulipa kodi kwa wakati.

Vilevile, katika makadirio ya kodi, baadhi ya wafanyabiashara walikuwa wakilalamikia kuwekewa makadirio makubwa tofauti na kiwango cha biashara zao. Hii iliweka uadui mkubwa kati ya TRA na walipakodi nchini.

MAGEUZI MAKUBWA YAMEONDOA UADUI KATI YA TRA NA WALIPAKODI

Kutokana na maelekezo ya Rais. Dk. Samia kwa TRA, uadui uliokuwepo awali kati ya TRA na walipakodi umeondoka. Hii inatokana na mtazamo chanya alioujenga Rais Dk. Samia kwa pande zote mbili.

Kimsingi, pande zote mbili zinategemeana. TRA anamtegemea mlipakodi kwani pindi kodi inapolipwa ndipo inawezesha utekelezaji wa miradi ya maendeleo ambayo inamnufaisha mlipakodi moja kwa moj.

Rais Dk. Samia akasisitiza pawepo na meza ya mazungumzo na makubaliano ya namna gani mlipakodi atalipa kodi pale ambapo atashindwa kulipa kwa wakati.

Aidha, Rais Samia akasisitiza kuwa kufunga biashara ni kummaliza kabisa mlipakodi kwani biashara yake itakapofungwa, ndipo atashindwa kabisa kulipa kodi kwani hatakuwa na shughuli ya kumuingizia kipato cha kuwezesha kulipa kodi na wala TRA haitaweza kupata kodi yake.

Kongole kwa Kamishna Mkuu wa TRA, Yusuph Mwenda, pamoja na wasaidizi wake nchi nzima wamefanyia kazi maelekezo ya Rais, na sasa tunashuhudia mafanikio ya kumalizika kwa uadui uliokuwepo awali.

Ni faraja kuona tunapoadhimisha miaka 30 ya TRA, kumejengeka uhusiano mzuri kati ya mlipakodi na mamlaka. Hakuna mabavu wala ubabe. Uhusiano mzuri uliopo umewezesha kuongezeka kwa mapato ya serikali.

Mathalani, mwezi Machi, 2026, TRA wamefanikiwa kukusanya trilioni 3.58, na kimsingi, ongezeko la makusanyo yamewezesha hata bajeti ya mwaka 2026/2027, kutegemea mapato ya ndani kwa asilimia 74.2.


Maoni : 0620 800 462


Na Janeth Raphael MichuziTv 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI), Prof. Riziki Shemdoe, ametoa maagizo ya kuchukuliwa hatua kwa maafisa rasilimali watu watakaobainika kusababisha ucheleweshaji wa upandishaji madaraja kwa watumishi wa umma, licha ya wahusika hao kutimiza vigezo vyote vinavyohitajika.

Prof. Shemdoe ametoa kauli hiyo leo wakati akifunga Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma jijini Dodoma, kwa niaba ya Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Dkt. Moses Kusiluka.

Amesema kumekuwepo na changamoto ya baadhi ya maafisa rasilimali watu kushindwa kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi, hali inayosababisha watumishi stahiki kukosa au kucheleweshwa kupanda madaraja kupitia mifumo ya kiutumishi.

“Watumishi wanaostahili kupandishwa vyeo hawapaswi kukosa haki zao kutokana na uzembe wa kiutendaji wa mtu mmoja,” amesisitiza.

Katika hatua nyingine, Prof. Shemdoe ameeleza kuwa hata yeye binafsi aliwahi kukumbana na changamoto ya kucheleweshwa kupandishwa cheo kwa takribani mwaka mmoja kutokana na kutokukamilika kwa taratibu za kiutumishi kwa wakati.

Aidha, ameelekeza kufanyika kwa tathmini maalum kwa maafisa rasilimali watu wakuu wote waliohusika na ucheleweshaji wa upandishaji madaraja katika mwaka wa fedha 2025/2026, ili hatua stahiki zichukuliwe dhidi ya waliobainika na uzembe.

Prof. Shemdoe pia amewataka waajiri kuhakikisha wanatenga bajeti ya kushiriki Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma, huku akisisitiza umuhimu wa maonesho hayo katika kuboresha utoaji huduma kwa wananchi.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora (OR-MUUUB), Bw. Juma Mkomi, amesema maadhimisho hayo ni sehemu ya utekelezaji wa azimio la Umoja wa Afrika linalolenga kuenzi Siku ya Utumishi wa Umma Barani Afrika.

Ameongeza kuwa lengo la maadhimisho hayo ni kutambua mchango wa watumishi wa umma katika maendeleo ya taifa, kuhamasisha ubunifu katika utoaji huduma, pamoja na kukusanya maoni ya wananchi kuhusu ubora wa huduma zinazotolewa na taasisi za umma.









-TASAC, ZMA Zaongeza Juhudi Kutatua Changamoto za Mabaharia

Na Mwandishi Wetu ,Kigoma

Serikali imesema itaendelea kuchukua hatua za kisera na kiutendaji ili kuboresha ustawi wa mabaharia nchini, ikiwemo kulinda haki zao za ajira, kuboresha mazingira ya kazi na kuhakikisha wanapata stahiki zao kwa wakati, kutokana na mchango wao mkubwa katika kukuza uchumi wa bluu.

Kauli hiyo imetolewa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Mhandisi Ali Said Bakar, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, wakati wa ufunguzi wa Maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani yaliyofanyika mkoani Kigoma.

Mhandisi Bakar alisema mabaharia ni sehemu muhimu ya maendeleo ya sekta ya usafirishaji wa majini na uchumi wa taifa kwa ujumla, hivyo ni lazima changamoto zinazowakabili zipatiwe ufumbuzi wa haraka na wa kudumu.

Alisema Serikali inatambua kuwa baadhi ya mabaharia wamekuwa wakikumbana na changamoto mbalimbali ikiwemo kunyanyaswa kazini, mishahara kutolipwa kwa wakati, ujira mdogo na ukosefu wa huduma muhimu kama bima na matibabu, hali inayohitaji usimamizi madhubuti kutoka kwa mamlaka husika.

“Maadhimisho haya yanatoa fursa ya kutafakari mchango wa mabaharia katika maendeleo ya nchi na kuonyesha dhamira ya Serikali ya kushughulikia changamoto zao kupitia sera, sheria na hatua za vitendo,” alisema.

Aidha, alizitaka taasisi zinazosimamia sekta ya usafirishaji wa majini kuhakikisha zinakuwa mstari wa mbele katika kusimamia haki za mabaharia, ikiwemo upatikanaji wa bima, huduma za afya na mazingira salama ya kazi.

Kwa upande wake, Katibu Tawala wa Mkoa wa Kigoma, Hassan Rugwa, alisema kufanyika kwa maadhimisho hayo mkoani humo ni ishara ya kutambua mchango wa Kigoma katika usafirishaji wa majini na maendeleo ya uchumi wa bluu.

Alisema maboresho makubwa yaliyofanywa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika miundombinu ya usafiri wa majini yameongeza kwa kiasi kikubwa usafirishaji wa mizigo kupitia njia za maji.

“Maadhimisho ya Mabaharia kwa Kigoma yameaksi sekta ya usafirishaji ya zaidi ya asilimia 70 ya mizigo kusafirishwa kwa kutumia njia za maji katika Mkoa wa Kigoma  jambo ambalo limeongeza umuhimu wa mabaharia katika uchumi wa taifa,” alisema Rugwa.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Bahari Zanzibar (ZMA), Fatma Said Sandali, alisema ZMA kwa kushirikiana na Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC) kuendelea kuweka mifumo bora ya uratibu na usimamizi ili kutatua changamoto zinazowakabili mabaharia.

Alisema maadhimisho hayo pia ni sehemu ya kuenzi mchango wa mabaharia waliopoteza maisha wakiwa kazini na kuonyesha mshikamano kwa familia zao.

Sandali alibainisha kuwa katika kipindi cha maadhimisho hayo, wananchi watapatiwa elimu kuhusu taaluma ya ubaharia, fursa zilizopo katika sekta ya usafirishaji wa baharini na maziwa, pamoja na umuhimu wa kuzingatia misingi ya kazi yenye utu, weledi na usalama.

Aliwataka mabaharia kuendelea kuzingatia nidhamu, uzalendo na taaluma katika kutekeleza majukumu yao, akieleza kuwa dunia ya sasa inahitaji mabaharia wenye ujuzi wa hali ya juu na weledi wa kimataifa.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya TASAC, Nahodha Mussa Mandia, alisema mabaharia ni nguzo muhimu ya sekta ya usafirishaji duniani na wanastahili kupewa kipaumbele katika mipango ya maendeleo.

Alisema Serikali imeendelea kufanya uwekezaji mkubwa katika sekta ya usafirishaji wa majini, ikiwemo ujenzi wa Bandari ya Kisasa ya Kalema mkoani Katavi, ambayo inatarajiwa kuongeza biashara na kuchochea ukuaji wa uchumi wa bluu nchini.

Mandia alisisitiza kuwa pamoja na kutambua mchango wa mabaharia, ni muhimu kwao kuendelea kufuata sheria, kanuni na taratibu za kazi ili kuongeza tija, usalama na ushindani wa sekta hiyo.

Maadhimisho ya Siku ya Mabaharia Duniani mwaka huu yanatarajiwa kuhusisha utoaji wa elimu katika mialo ya uvuvi, shule na maeneo mbalimbali ya jamii kwa lengo la kuongeza uelewa kuhusu mchango wa mabaharia katika maendeleo ya uchumi wa Tanzania.

Katibu Mkuu wa Wizara Ujenzi na Uchukuzi  Zanzibar Mhandisi Ali Said Bakar akipokea zawadi kutoka kwa Mwenyekiti wa Bodi ya TASAC Nah.Mussa Mandia mara baada ya  kufungua  Maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani mkoani  Kigoma .
Katibu Mkuu wa Wizara Ujenzi na Uchukuzi  Zanzibar Mhandisi Ali Said Bakar akizungumza katika Ufunguzi wa  maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani mkoani  Kigoma .




Matukio mbalimbali katika picha wakati wa ufunguzi wa Maadhimisho ya 16 ya Siku Mabaharia Duniani.


Na Victor Masangu,Pwani


Mamlaka ya mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Pwani katika kipindi cha miaka kumi iliyopita kuanzia mnamo mwaka 2015 hadi mwaka 2026 imefanikiwa kufanya vizuri baada ya kukusanya kodi kiasi cha shilingi bilioni 266.

Hayo yamebainishwa na Meneja wa TRA Mkoa wa Pwani Peter Eliona wakati wa halfa ya kongamano maalumu ambalo limewajumuisha wadau mbali mbali pamoja na walipa kodi ikiwa ni katika kuelekea maadhimisho ya miaka 30 ya TRA.

Meneja huyo amebainisha kwamba fedha hizo zimekusanywa kutokana na kuwepo kwa mfumo mizuri waliyoiweka katika suala zima la ukusanyaji ikiwemo pamoja na kuwashirikisha walipa kodi.

Aidha meneja huyoo amesema kwamba lengo kubwa TRA ni kuendelea kuweka mikakati ya kuendelea kukusanya kodi ambayo imekuwa ni mkombozi katika kutekeleza miradi mbali mbali ya maendeleo.

"Leo tumekutana katika kongamano hili ambalo tumeweza kuwashirikisha sadau wetu wa maendeleo pamoja na walipa kodi ili kuweza kujadili mambo mbali mbali ya ulipaji wa kodi,"amebainisha Meneja huyo.

Naye Mwenywkiti wa Chama cha Wafanyabiashara Mkoa wa Pwani Abdallah Ndauka amesema ili kuongeza makusanyo TRA wanatakiwa kuangalia namna ya kuwasaidia wafanyabiashara wasifunge biashara zao badala yake wajikite kushauri kuwasaidia kuendelea zaidi.

Amesema kwamba wapo wafanyabiashara wanafunga biashara zao kutokana na sababu mbalimbali ili kunusuru hilo ni vema watumishi wa Mamlaka hiyo wakawa msaada wa kuzifufua ili waendelee kupata kodi.

Pia, ameiomba TRA mkoa wa Pwani kuwa sehemu ya kutoa fursa kwa wafanyabiashara hao ili kukuza biashara zao kwa kununua vifaa na samani nyingine badala ya kuagiza nje ya nchi.

Mamlaka ya Mapato (TRA)) Mkoa wa Pwani imekuwa ikishirikiana bega kwa bega na walipa kodi pamoja na kutoa mafunzo ambayo yamesaidia kuongeza kasi ya ukusanyaji wa mapato na kuvuka malengo.


Na Mwandishi Wetu, Kigoma

Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC), Mohamed Salum, amesema kuwa usafiri wa meli ya MV Liemba una umuhimu mkubwa kwa wananchi wanaotegemea huduma za usafiri wa majini katika ukanda wa Ziwa Tanganyika, huku akieleza kuwa meli hiyo itakuwa chachu ya maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

Salum alitoa kauli hiyo wakati alipotembelea eneo la ujenzi wa meli ya MV Liemba mjini Kigoma katika maadhimisho ya Siku ya Mabaharia yanayoendelea mkoani humo.

Amesema kuwa wananchi wengi wa maeneo yanayozunguka Ziwa Tanganyika wanategemea usafiri wa majini kwa shughuli mbalimbali za kijamii na kiuchumi, hivyo kukamilika kwa ujenzi wa meli hiyo kutasaidia kuboresha huduma za usafiri na usafirishaji wa bidhaa.

“Meli ya MV Liemba ni muhimu kwa wananchi wetu kwa sababu inatoa huduma zinazogusa maisha ya kila siku ya watu wengi. Kukamilika kwake kutaimarisha usafiri salama na wa uhakika katika maeneo yanayohudumiwa na meli hiyo,” amesema Salum.

Aliongeza kuwa katika mkoa wa Kigoma, MV Liemba itaendelea kuwa nyenzo muhimu ya kuchochea shughuli za biashara, kuunganisha jamii na kurahisisha upatikanaji wa huduma mbalimbali za kijamii kwa wananchi wa ukanda huo.

Salum amesema uwekezaji unaofanyika katika kuboresha meli hiyo unaonesha dhamira ya Serikali ya kuimarisha sekta ya usafiri wa majini na kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora zinazochangia ukuaji wa uchumi wa bluu nchini.

Ziara hiyo ni sehemu ya shughuli za Maadhimisho ya Siku ya Mabaharia ambayo yanalenga kutambua mchango wa mabaharia na wadau wa sekta ya usafiri wa majini katika maendeleo ya taifa.



Wataalamu wa afya, watafiti, viongozi wa vijana na wadau mbalimbali wa maendeleo kutoka ndani na nje ya Afrika wamekutana jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kujadili namna ya kuimarisha huduma na sera za afya kwa vijana balehe barani Afrika.

Kwa mujibu wa taarifa kwa umma iliyotolewa na Mtandao wa ARISE kupitia Mkurugenzi Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Afrika ya Afya ya Umma, Dkt. Mary Mwanyika Sando, Juni 22, 2026, inaeleza kuwa Mkutano wa 2026 wa Afya ya Vijana Balehe Kusini mwa Jangwa la Sahara (CAH-SSA) pamoja na Mikutano ya Mwaka ya Mtandao wa Utafiti, Sayansi ya Utekelezaji na Elimu Afrika (ARISE), unafanyika kuanzia Juni 22 hadi 25, 2026 Jijini Dar es Salaam.

Mkutano huo unafanyika chini ya kaulimbiu “Kuonesha Mafanikio ya Afua Endelevu za Afya ya Vijana Balehe Zinazoongozwa na Jamii”, ukiwa na lengo la kuonesha matokeo ya tafiti na kujadili mbinu bora za kuboresha afya ya vijana.

Mgeni rasmi katika mkutano huo ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya Tanzania, Dkt. Seif Abdallah Shekalaghe, ambaye amezungumzia namna matokeo ya tafiti yanavyoweza kutumika kuboresha sera za afya, kuimarisha huduma kwa vijana na kuongeza ushiriki wa vijana katika ubunifu na utekelezaji wa afua zinazowahusu.

Mkutano huo umewakutanisha wadau mbalimbali wakiwemo Serikali, washirika wa maendeleo, viongozi wa vijana, watafiti, taasisi za utafiti na sekta binafsi kwa lengo la kujenga ushirikiano wa kuongeza matokeo chanya katika afya ya vijana barani Afrika.

Katika mkutano huo, vijana pia wamepewa nafasi kupitia Wawakilishi wa Bodi ya Ushauri ya Vijana Balehe na Vijana kwa ujumla (AYAB), akiwemo Mtanzania Bi. Mariam Surve na Bi. Mariam Yusuff kutoka Nigeria, ambao wanawakilisha sauti na mahitaji ya vijana katika uundaji na utekelezaji wa programu za afya.

Miongoni mwa maeneo yatakayojadiliwa ni matokeo ya miradi ya DASH na ARISE-NUTRINT inayolenga kuboresha afya ya vijana katika maeneo ya lishe, mazoezi, afya ya uzazi na afya ya akili. Miradi hiyo imefadhiliwa na Serikali ya Ujerumani pamoja na Umoja wa Ulaya.

Aidha, mkutano huo unalenga kuimarisha mipango ya Mtandao wa ARISE kwa kipindi cha mwaka 2026–2027 kwa kuweka mikakati itakayowezesha afua za afya kwa vijana kuwa endelevu kifedha na kutekelezwa kwa upana katika ngazi za jamii, kitaifa na kikanda.

Wakizungumza kuhusu umuhimu wa mkutano huo, viongozi wa ARISE wamesema jukwaa hilo ni muhimu katika kuunganisha tafiti, matokeo yake, sera na utekelezaji wa programu zinazolenga kuboresha maisha ya vijana barani Afrika.

Mtandao wa ARISE ni ushirikiano wa taasisi za Afrika na mabara mengine unaolenga kuimarisha uwezo wa utafiti wa afya ya umma na kuendeleza utekelezaji wa afua zenye msingi wa ushahidi, ukiwa na zaidi ya taasisi 22 kutoka nchi mbalimbali Kusini mwa Jangwa la Sahara.










Na Oscar Assenga, Muheza

WANANCHI 6,258 wa Kijiji cha Muungano, Wilaya ya Muheza, wamenufaika na huduma bora za afya kufuatia kukamilika kwa ujenzi wa Zahanati ya Muungano, mradi ambao umepokelewa na kuridhiwa na Mwenge wa Uhuru 2026 baada ya kukaguliwa na kupokea taarifa ya utekelezaji wake.

Akizungumza wakati wa ukaguzi wa mradi huo, Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2026 Wazo Mwang'onda alisema kukamilika kwa zahanati hiyo kumesaidia kusogeza huduma za matibabu karibu na wananchi na kupunguza changamoto ya kusafiri umbali mrefu kufuata huduma za afya.

Alisema Serikali tayari imepeleka vifaa tiba pamoja na watumishi wa afya watakaotoa huduma katika zahanati hiyo, hatua inayoonesha dhamira ya kuboresha upatikanaji wa huduma za afya, hususan katika maeneo ya vijijini.

“Mradi huu ni muhimu kwa wananchi wa Muungano na maeneo jirani kwa sababu unasaidia kuboresha upatikanaji wa huduma za afya na kuongeza ustawi wa jamii,” alisema.

Kiongozi huyo aliongeza kuwa mafanikio ya mradi huo yametokana na ushirikiano kati ya Serikali na wadau wa maendeleo, hususan Taasisi ya Islamic Help, iliyochangia ujenzi wa zahanati hiyo, huku Serikali ikigharamia vifaa tiba na watumishi wa afya.

Aliwashukuru wadau wa maendeleo kwa kuendelea kushirikiana na Serikali katika utekelezaji wa miradi ya kijamii, na kuwataka kuendeleza ushirikiano huo ili kusaidia kuboresha huduma muhimu kwa wananchi.

Aidha, aliwahimiza wananchi kuendelea kulinda amani na utulivu wa nchi, akisema kuwa mazingira hayo yanawezesha utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kuvutia wadau zaidi kushirikiana na Serikali.

Kwa upande wake, akitoa taarifa ya mradi huo, Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Wilaya ya Muheza, Dk. Fani Mussa, alisema ujenzi wa Zahanati ya Muungano ulianza Machi 2, 2025 na kukamilika kwa gharama ya Shilingi milioni 165.94.

Alieleza kuwa kati ya fedha hizo, Shilingi milioni 141.55 zilitumika kwa ujenzi, huku Shilingi milioni 24.39 zikitumika kununua vifaa tiba.

Kwa mujibu wa Dk. Mussa, zahanati hiyo itahudumia wakazi 6,258 wa Kijiji cha Muungano, wakiwemo wanaume 3,089 na wanawake 3,169, na inatarajiwa kwa kiasi kikubwa kuboresha upatikanaji wa huduma za afya katika eneo hilo.

Baada ya ukaguzi huo, Mwenge wa Uhuru 2026 ulieleza kuridhishwa na ubora wa utekelezaji wa mradi huo, ukibainisha kuwa ni hatua muhimu katika kusogeza huduma za afya karibu na wananchi na kuunga mkono jitihada za Serikali za kuimarisha sekta ya afya nchini.




Top News