Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga, amesema Serikali imebadili mtazamo katika kusimamia sekta ya viwanda na biashara kwa kuweka mkazo kwenye uwezeshaji badala ya udhibiti, akisisitiza kuwa taasisi zilizo chini ya wizara hiyo hazitakuwa “polisi wa biashara” bali washirika wa biashara katika kukuza uchumi wa taifa.

Akichangia hoja ya Bajeti Kuu ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2026/2027 Bungeni jijini Dodoma Juni 22, 2026, Mhe. Kapinga amesema sekta ya viwanda na biashara ndiyo nguzo muhimu ya kufanikisha Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kutokana na uwezo wake wa kuzalisha ajira kwa vijana, kuongeza pato la taifa, kuharakisha matumizi ya teknolojia na kuimarisha biashara ya kimataifa.

Amesema wabunge wamejadili kwa kina umuhimu wa kuanzisha viwanda vipya vya kimkakati, kuvilinda viwanda vilivyopo, kuongeza ajira kwa vijana na kuimarisha mazingira ya biashara, huku Serikali ikiahidi kuyafanyia kazi mapendekezo yote yaliyotolewa.

Mhe. Kapinga amesema Bajeti ya mwaka 2026/2027 imeweka mazingira rafiki kwa wawekezaji kupitia punguzo la kodi kwa viwanda vipya, unafuu wa kodi kwenye mitambo na vifaa vya uzalishaji, pamoja na kupunguza ushuru kwa malighafi zinazotumika viwandani.

Ameeleza kuwa taasisi 13 zilizo chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara, zikiwemo TBS na BRELA, zina jukumu la kufungua fursa za biashara na siyo kuwa kikwazo cha ukuaji wa sekta hiyo “Sisi siyo mgambo wala polisi wa biashara, Tunataka kuwa marafiki wa wafanyabiashara, kuwaelekeza, kuwawezesha na kujenga mazingira bora ya kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.”


Kampuni ya Mbolea Tanzania (TFC) imesema ipo katika hatua za Kuzindua kiwanda cha kisasa cha kuchakata mbolea Mkoani Tanga kitakachozalisha mbolea kulingana na kiwango cha rutuba ya udongo wa maeneo mbalimbali nchini, hatua inayolenga kuongeza tija kwa wakulima na uzalishaji wa mazao.

Akizungumza na waandishi wa habari katika kilele cha maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma jijini Dodoma Juni 23, 2026, Mkurugenzi wa Huduma za Taasisi wa TFC, Nuru Mhando, kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa kampuni hiyo, amesema kiwanda hicho kinatarajiwa kujengwa mkoani Tanga na kitakuwa na uwezo wa kuzalisha mbolea zinazokidhi mahitaji halisi ya udongo wa kila eneo.

Amesema kupitia teknolojia ya upimaji wa udongo, kiwango cha rutuba kitafahamika kabla ya kutengenezwa mbolea maalum inayofaa kwa eneo husika, jambo litakalosaidia kuongeza uzalishaji wa mazao kwa ufanisi zaidi.

“Kiwanda hiki kitazalisha mbolea kulingana na mahitaji ya udongo wa maeneo tofauti nchini, hii itasaidia wakulima kupata mbolea sahihi na kuongeza mavuno kwa gharama nafuu.”

Ameeleza kuwa kuanzishwa kwa kiwanda hicho kutapunguza utegemezi wa mbolea kutoka nje ya nchi na kupunguza gharama za uagizaji, huku kikichangia upatikanaji wa mbolea bora kwa wakati unaohitajika.

Mhando amesema TFC ni kampuni ya serikali inayosambaza mbolea kwa wakulima kupitia mfumo wa ruzuku, ambapo serikali huchangia sehemu ya gharama za mbolea ili kuwasaidia wakulima kuzipata kwa bei nafuu.

Amesema kampuni hiyo imeendelea kusambaza mbolea za mazao ya chakula na nafaka, ambapo hadi sasa zaidi ya tani 49,000 za mbolea za kupandia na kukuzia mazao zimesambazwa kwa wakulima nchini, pia imekuwa ikitoa mbolea kwa wakulima wa tumbaku, moja ya mazao ya kimkakati nchini.

Aidha, amesema TFC inaendelea kutoa mafunzo kwa wakulima kuhusu matumizi sahihi ya mbolea ili kuongeza ufanisi katika uzalishaji na kuhakikisha pembejeo hizo zinatumika kwa manufaa makubwa.

Amesisitiza kuwa kampuni hiyo itaendelea kutoa elimu na kutatua changamoto zinazowakabili wakulima ili kuongeza uzalishaji wa mazao ya chakula na biashara, hatua itakayochangia upatikanaji wa chakula cha kutosha na kuimarisha uchumi wa wananchi.



Mamlaka ya Udhibiti wa Mkondo wa Juu wa Petroli (PURA) imesema matumizi ya gesi asilia nchini yameongezeka kwa kiwango kikubwa kutokana na kampeni ya matumizi ya nishati safi ya kupikia, hali inayochochea maendeleo ya sekta ya mafuta na gesi pamoja na kuongeza manufaa kwa wananchi.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma Juni 23, 2026, katika kilele cha maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma, Mkurugenzi Mkuu wa PURA, Eng. Charles Sangweni, amesema ongezeko hilo limechangiwa na juhudi za Serikali zinazoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan za kuhamasisha matumizi ya nishati safi na rafiki kwa mazingira.

Eng. Sangweni amesema mwenendo wa matumizi ya nishati duniani unaonesha kuwa katika miaka ijayo matumizi ya mafuta ya petroli na dizeli yanaweza kupungua kutokana na maendeleo ya teknolojia na ongezeko la matumizi ya magari ya umeme pamoja na yale yanayotumia gesi asilia.

Amesema hali hiyo inaifanya gesi asilia kuwa rasilimali muhimu zaidi katika kipindi hiki cha mpito huku Tanzania ikiwa na fursa kubwa ya kunufaika kutokana na akiba yake ya gesi na mahitaji yanayoendelea kuongezeka katika soko la ndani na nje ya nchi.

Ameeleza kuwa pamoja na mabadiliko ya teknolojia duniani yanayochochea matumizi ya magari ya umeme na yale yanayotumia gesi asilia, Tanzania bado ina nafasi kubwa ya kunufaika na rasilimali zake kutokana na mahitaji yanayoendelea kuongezeka.

Sangweni amesema PURA imeendelea kupata mafanikio makubwa tangu kuanzishwa kwake kwa kusimamia utekelezaji wa mikataba ya utafutaji, uchimbaji na uzalishaji wa mafuta na gesi, hatua ambayo imechangia kuongeza mapato ya serikali kupitia mirabaha, kodi na vyanzo vingine vya mapato.

Aidha, amesema wananchi wanaendelea kunufaika kupitia utekelezaji wa sera za maudhui ya ndani (Local Content), ambapo Watanzania wanapewa kipaumbele katika zabuni za huduma, bidhaa na ajira zinazotokana na shughuli za sekta ya mafuta na gesi.

Amesisitiza kuwa PURA itaendelea kusimamia kwa karibu shughuli zote za utafutaji na uzalishaji wa mafuta na gesi ili kuhakikisha rasilimali hizo zinatumika kwa manufaa ya taifa na kuchangia mapato.


Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Prof. Godius Kahyarara, Juni 22, 2026 alitembelea banda la Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) katika Maonesho ya Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma, yanayofanyika katika viwanja vya Chinangali Park, jijini Dodoma.

Akiwa katika banda hilo, Prof. Kahyarara alipokewa na Meneja wa TCAA Kituo cha Dodoma, Aswile Kamendu, ambaye alimueleza juhudi mbalimbali zinazotekelezwa na Mamlaka katika kuimarisha sekta ya usafiri wa anga nchini, ikiwemo maboresho ya miundombinu ya anga, kuimarisha usalama wa safari za anga pamoja na kuhimiza matumizi ya teknolojia za kisasa katika utoaji wa huduma.

Akizungumza mara baada ya kutembelea banda hilo, Prof. Kahyarara alisema: “Serikali inaendelea kuwekeza katika kuimarisha sekta ya usafiri wa anga kwa kuhakikisha miundombinu inaboreshwa, usalama unaimarishwa na teknolojia za kisasa zinatumika ili kuongeza ufanisi wa huduma. Hatua hizi ni muhimu katika kuchochea maendeleo ya uchumi na kuimarisha ushindani wa nchi yetu kikanda na kimataifa.”

Mbali na Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, wageni wengine waliotembelea banda la TCAA ni pamoja na Katibu Mkuu Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bw. Juma Mkomi, Mkuu wa Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima (TEWW), Prof. Philipo Sanga, na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini (LATRA), Dkt. Habibu J. Suluo, na kupata maelezo kuhusu majukumu ya Mamlaka, mafanikio yaliyopatikana pamoja na mikakati inayotekelezwa katika kuimarisha usalama, ufanisi na maendeleo ya sekta ya usafiri wa anga nchini.

Kupitia ushiriki wake katika maonesho hayo, TCAA inatumia fursa hiyo kuwahamasisha vijana na wadau wa sekta ya usafiri wa anga kuchangamkia fursa za mafunzo zinazotolewa na Chuo cha Usafiri wa Anga Tanzania (CATC), chuo kinachomilikiwa na TCAA. Mafunzo yanayotolewa chuoni hapo yanalenga kukabiliana na changamoto ya upungufu wa wataalamu wa ndani katika sekta ya usafiri wa anga kwa kuzalisha wataalamu wa kutosha na wenye viwango vinavyokubalika kimataifa.

Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma mwaka huu yanaongozwa na kaulimbiu isemayo “Kuchochea Uwajibikaji Jumuishi kwa Huduma Endelevu”, ikisisitiza umuhimu wa matumizi ya teknolojia katika kuboresha huduma kwa wananchi na kuimarisha uwajibikaji katika utumishi wa umma.

Wiki ya Utumishi wa Umma huadhimishwa kila mwaka kwa lengo la kutambua mchango wa watumishi wa umma katika maendeleo ya taifa, ambapo maadhimisho ya mwaka huu yanatarajiwa kufikia kilele chake Juni 23, 2026.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Prof. Godius W. Kahyarara akisaini kitabu katika banda la Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) kwenye maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayofanyika katika viwanja vya Chinangali Park, jijini Dodoma.
Meneja wa TCAA Kituo cha Dodoma Aswile Kamendu akitoa maelezo kwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Prof. Godius W. Kahyarara aliyefika katika banda la Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) kwenye maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayofanyika katika viwanja vya Chinangali Park, jijini Dodoma.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Prof. Godius W. Kahyarara akipokea zawadi kutoka kwa Meneja wa TCAA Kituo cha Dodoma Aswile Kamendu alipotembelea banda la Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) kwenye maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayofanyika katika viwanja vya Chinangali Park, jijini Dodoma.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Prof. Godius W. Kahyarara akizungumza jambo katika banda la Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) kwenye maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayofanyika katika viwanja vya Chinangali Park, jijini Dodoma.
Katibu Mkuu Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bw. Juma Mkomi akisaini kitabu katika banda la Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) kwenye maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayofanyika katika viwanja vya Chinangali Park, jijini Dodoma.



Katibu Mkuu Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bw. Juma Mkomi akiwa kwenye picha ya pamoja na Watumishi wa TCAA alipotembelea katika banda la Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) kwenye maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayofanyika katika viwanja vya Chinangali Park, jijini Dodoma.
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini (LATRA), Dkt. Habibu J. Suluo akisaini kitabu katika banda la Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) kwenye maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayofanyika katika viwanja vya Chinangali Park, jijini Dodoma.


Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini (LATRA), Dkt. Habibu J. Suluo akizungumza jambo alipotembelea banda la Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) kwenye maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayofanyika katika viwanja vya Chinangali Park, jijini Dodoma.


Mkuu wa Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima (TEWW), Prof. Philipo Sanga akisaini kitabu katika banda la Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) kwenye maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayofanyika katika viwanja vya Chinangali Park, jijini Dodoma.



Afisa Rasilimali Watu TCAA Lucy Ngowo (wa pili kulia) akikabidhi zawadi kwa Mkuu wa Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima (TEWW), Prof. Philipo Sanga alipotembelea banda la Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) kwenye maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayofanyika katika viwanja vya Chinangali Park, jijini Dodoma.

Na Janeth Raphael MichuziTv - Bungeni Dodoma

Serikali ya Tanzania inaendelea kuchukua hatua kubwa za kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji kupitia uanzishaji wa Mfumo wa Kidigitali wa One Stop Centre unaolenga kuunganisha taasisi mbalimbali za umma katika kutoa huduma kwa wawekezaji kwa njia rahisi na ya kisasa.

Akijibu swalibungeni leo, Naibu Nchi, Ofisi ya Rais (Mipango na Uwekezaji) Dkt. Pius Chaya amesema mfumo huo unatekelezwa kwa awamu mbili, lengo likiwa ni kurahisisha upatikanaji wa huduma, kupunguza urasimu na kuongeza ufanisi katika sekta ya uwekezaji nchini.

Amefafanua kuwa awamu ya kwanza ya mfumo huo tayari imekamilika ambapo taasisi muhimu zimeunganishwa, zikiwemo Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA), Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) na Idara ya Uhamiaji. Kupitia muunganiko huo, huduma kama usajili wa miradi ya uwekezaji, uhakiki wa kampuni, uhakiki wa vitambulisho vya taifa na uhakiki wa pasipoti sasa zinafanyika kwa mfumo mmoja wa kidigitali kwa ufanisi zaidi.

Aidha, serikali imeeleza kuwa awamu ya pili ya utekelezaji itapanua zaidi mfumo huo kwa kuunganisha huduma nyingine muhimu ikiwemo usajili wa kampuni, vibali vya makazi, namba ya utambulisho wa taifa (NIN), namba ya mlipakodi (TIN), msamaha wa kodi pamoja na vibali vya kazi. Hatua hiyo inalenga kuhakikisha wawekezaji wanapata huduma zote muhimu kupitia sehemu moja ya kidigitali.

Serikali imesisitiza kuwa lengo kuu la mfumo huo ni kuboresha mazingira ya biashara nchini kwa kupunguza muda wa mchakato wa kupata huduma, kupunguza gharama na kuongeza uwazi na ufanisi katika utoaji wa huduma kwa wawekezaji wa ndani na nje ya nchi.

Kwa ujumla, Mfumo wa One Stop Centre unatarajiwa kuwa chachu ya kuvutia uwekezaji zaidi nchini kupitia huduma jumuishi za kidigitali zinazowezesha urahisi wa kufanya biashara.


Na Mwandishi Wetu 

NAIBU Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Dkt. Ngwaru Maghembe ameshiriki Mkutano wa Dharura wa Mawaziri wa Utatu wa Asasi ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC Organ Troika) uliofanyika kwa njia ya mtandao kujadili hali ya usalama katika kanda.

Akimwakilisha Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dkt. Maghembe aliipongeza SADC kwa juhudi za kuimarisha amani, usalama na kusuluhisha migogoro inayoibuka katika kanda.

Aidha, alisisitiza kuwa Tanzania itaendelea kuunga mkono juhudi za SADC katika kuimarisha amani kwenye ukanda huo.

Utatu wa Asasi ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya SADC inaundwa na Nchi za Malawi Mwenyekiti, Eswatini Mwenyekiti ajaye na Tanzania Mwenyekiti anayemaliza muda wake na ina jukumu la kulinda kusimamia na kuhakikisha amani, usalama na utulivu unatamalaki katika ukanda wa SADC.





Na Janeth Raphael MichuziTv -  Bungeni Dodoma 

Serikali imesema imebaini kuwepo kwa vitendo vya ujanja ujanja katika sekta ya ajira nchini, hali inayochangia kukiuka sheria na taratibu za ajira pamoja na kuathiri haki za wafanyakazi.

Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano ya Kazi), Dkt, Eveline Munisi, ameeleza hayo leo Bungeni jijini Dodoma wakati akijibu swali la Mbunge wa Nyasa, John John Nchimbi, aliyetaka kufahamu mpango wa serikali wa kuwasaidia Kamishna wa Kazi ili waweze kuwa na programu maalum za kutoa elimu katika maeneo mbalimbali, hususan migodini, ili kuelimisha kuhusu madhara ya ajira za watoto wadogo.

Mbunge huyo pia alihoji juu ya changamoto ya wageni wanaofanya kazi nchini bila kuwa na uelewa wa kutosha wa sheria za kazi, akisisitiza umuhimu wa kupatiwa elimu ya msingi kuhusu taratibu hizo.

Akijibu hoja hizo, Naibu Waziri Dkt. Munisi amesema serikali imebaini uwepo wa baadhi ya watu wanaofanya udanganyifu katika mchakato mzima wa ajira, ambapo “vishoka” huwachukua wananchi na kuwapangisha kazi kinyume na sheria na taratibu zilizowekwa.

Amesema serikali ipo katika hatua za kuimarisha utoaji wa elimu kwa waajiri, taasisi na wadau mbalimbali ili kuhakikisha wanazingatia sheria za kazi na kulinda haki za wafanyakazi, hususan makundi yaliyo katika mazingira hatarishi.

Aidha, amesisitiza kuwa serikali haitasita kuchukua hatua kali za kisheria dhidi ya wote watakaobainika kujihusisha na vitendo hivyo vinavyokiuka sheria za ajira nchini.




JUMLA ya vijiji vitatu katika mikoa ya Mtwara, Tanga, na Dodoma vimeanza kunufaika na huduma bora za kidijitali kufuatia hatua ya kampuni ya mawasiliano ya Airtel Tanzania kupanua miundombinu yake kwa kujenga minara mipya ya mawasiliano. Maeneo yaliyofaidika ni pamoja na Kijiji cha Chungu (Wilaya ya Nanyumbu), Kata ya Madanga (Wilaya ya Pangani), na Kijiji cha Pahi (Wilaya ya Kondoa).

Kwa miaka mingi, maeneo haya ya vijijini yalikabiliwa na changamoto sugu za mtandao usio na uhakika. Changamoto hiyo ilisababisha ugumu wa kupata huduma za intaneti na kurudisha nyuma shughuli za kijamii na kiuchumi, hasa katika sekta ya kilimo na biashara ndogondogo.

Katika Mkoa wa Mtwara, wakazi wa Kijiji cha Chungu walieleza kuwa wameishi bila huduma za uhakika za mawasiliano tangu kijiji hicho kilipoanzishwa mwaka 2004. Licha ya kuwa na idadi ya watu zaidi ya 2,400, eneo hilo lilikuwa na maeneo machache sana yenye mtandao, hali iliyowalazimu wakazi kutafuta sehemu maalum ili kupiga simu.

Mwenyekiti wa Kijiji hicho, Rajabu Zawadi Staudi, alisema hali hiyo ilikuwa ikivuruga maisha yao ya kila siku. “Kwa miaka mingi, huduma za mawasiliano zilipatikana kwa shida kwenye baadhi ya maeneo tu, na huduma ya intaneti haikuwepo kabisa,” alisema. Aliongeza kuwa mnara huo mpya unaleta matumaini mapya ya maendeleo vijijini, hasa katika kilimo na ajira kwa vijana.

Wakulima wa eneo hilo walisema kuimarika kwa mtandao kutawasaidia kusimamia vizuri mazao yao kama vile korosho, ufuta, mbaazi, karanga, mahindi, na mtama. Vilevile wanatarajia kupata urahisi wa kutumia huduma za kibenki kwa njia ya simu, kujua bei za masoko, na kutumia mifumo ya kidijitali inayochochea biashara ya kilimo.

Kwa upande wa Mkoa wa Tanga, wakazi wa Kata ya Madanga wilayani Pangani walieleza adha ya muda mrefu ya ukosefu wa mtandao, ambapo baadhi yao walilazimika kupanda juu ya miti au kwenda maeneo ya miinuko ili tu kupata mawasiliano.

Wakati wa uzinduzi wa huduma za Airtel katika eneo hilo, viongozi wa eneo hilo waliongoza sherehe za ukataji utepe kuashiria uboreshaji rasmi wa huduma za mawasiliano. Diwani wa Kata hiyo, Mungia Kiluwasha, na mkulima Ismail Zubeiry walisema mtandao huo mpya utarahisisha upatikanaji wa masoko na kuimarisha shughuli za kibiashara vijijini.

Meneja Biashara wa Airtel Mkoa wa Tanga, Nassor Laizer, alisema uwekezaji huo unalenga kusaidia maendeleo ya vijijini. “Hii ni fursa kubwa kwa wananchi kuboresha maisha yao ya kiuchumi kupitia mawasiliano bora na huduma za kidijitali,” alisema.

Katika Mkoa wa Dodoma, wakazi wa Kijiji cha Pahi wilayani Kondoa nao wamepongeza uboreshaji wa huduma za mtandao baada ya miaka mingi ya mawasiliano duni ambayo yalizuia upatikanaji wa huduma za kupiga simu, ujumbe mfupi (SMS), na intaneti.

Thomas Sharif Thomas, Meneja Mauzo wa Airtel Kanda ya Kondoa, alisema miundombinu hiyo mipya imeongeza ubora wa mawasiliano na kutengeneza fursa za ajira vijijini kupitia mitandao ya mawakala wa Airtel na huduma za usajili wa laini za simu.

Mwenyekiti wa Kijiji hicho, Shaibu Ali Omari, aliwasihi wakazi kuilinda miundombinu hiyo mipya ili kuhakikisha inaleta faida za muda mrefu.

Naye mfanyabiashara Ali Kamil alisema kuwa wakala wa Airtel kumemwongezea kipato kupitia huduma za kifedha za simu kama vile Lipa Namba, ambayo imerahisisha miamala vijijini.

Katika mikoa hiyo mitatu, wakazi sasa wanaona kuimarika kwa mtandao kama chachu kuu ya maendeleo. Wanaamini kuwa mtandao imara wa simu utaboresha kilimo, utapanua fursa za biashara, na kuziba pengo la kidijitali lililokuwepo kwa muda mrefu kati ya jamii za vijijini na mijini.



Na Mwandishi Wetu Zanzibar
YAS Fiber Tanzania itawekeza takriban shilingi bilioni 300 kwa kipindi cha miaka 20 ili kupanua huduma za intaneti yenye kasi visiwani Zanzibar kufuatia kusainiwa kwa makubaliano ya Ushirikiano kati ya kati ya Shirika la Mawasiliano Zanzibar (ZICTIA), Wizara ya Kazi na Uwekezaji Zanzibar na Yas Fiber.

Uwekezaji huo unatarajiwa kuwezesha huduma za mkonga wa mawasiliano (fiber) katika kuzifikia takriban kaya 100,000 katika visiwa vya Unguja na Pemba ndani ya miaka mitatu ya kwanza ya utekelezaji wa mradi.

Makubaliano hayo yanaashiria hatua muhimu katika juhudi za kuimarisha miundombinu ya kidigitali Zanzibar na kuongeza upatikanaji wa huduma za intaneti za uhakika, nafuu na zenye kasi kwa kaya, biashara, taasisi za elimu, vituo vya afya na taasisi za Serikali. Aidha, yanaunga mkono azma ya Zanzibar ya kujiimarisha kama kitovu cha ubunifu, uwekezaji na huduma za kidigitali.

Akizungumza wakati wa hafla ya utiaji saini wa makubaliano hayo, Waziri wa Mawasiliano, Teknolojia ya Habari na Ubunifu Zanzibar, Mhe. Mudrick Ramadhan Soraga, alisema ushirikiano huo unaonesha dhamira ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya kutumia teknolojia kama nyenzo ya kuharakisha maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

"Miundombinu ya kidigitali ni msingi wa uchumi wa kisasa. Ushirikiano huu utaharakisha mageuzi ya kidigitali na kusaidia kuiweka Zanzibar katika nafasi ya kuwa miongoni mwa vinara wa uchumi wa kidigitali katika ukanda wa Afrika Mashariki," alisema Mhe. Soraga.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa ZICTIA, Mhandisi Shukuru Awadh Suleiman, alisema makubaliano hayo yataongeza kasi ya upanuzi wa huduma ya mkonga wa mawasiliano visiwani humo na kusaidia kuimarisha upatikanaji wa huduma bora za mawasiliano kwa wananchi

"Ushirikiano huu utawezesha wananchi na taasisi nyingi zaidi kupata huduma za intaneti yenye kasi na kuchangia ujenzi wa miundombinu ya kidigitali inayohitajika kwa maendeleo ya Zanzibar ya sasa na ya baadae," alisema Mhandisi Suleiman.

Naye Afisa Mtendaji Mkuu wa Yas Fiber, Maxime Woimant, alisema uwekezaji huo unaonesha dhamira ya kampuni hiyo katika kuunga mkono ajenda ya mageuzi ya kidigitali nchini na maendeleo jumuishi kupitia mawasiliano ya kisasa."Huu ni miongoni mwa uwekezaji mkubwa zaidi wa miundombinu ya kidigitali kuwahi kufanyika Zanzibar katika miaka ya hivi karibuni.

Kupitia ushirikiano huu, tutapanua upatikanaji wa huduma za intaneti za viwango vya kimataifa zitakazowezesha biashara kukua, wanafunzi kujifunza, ubunifu kwa taasisi na jamii kushiriki kikamilifu katika uchumi wa kidigitali," alisema Woimant.

Aliongeza kuwa Yas Fiber inajiona si mwekezaji pekee bali mshirika wa maendeleo wa muda mrefu anayelenga kupanua fursa za kijamii na kiuchumi kupitia mawasiliano ya uhakika na ya kisasa.Mradi huo utatekelezwa chini ya mfumo wa Ushirikiano kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP), ukiunganisha maono ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya kujenga uchumi wa kidigitali na uzoefu wa Yas Fiber katika kubuni, kuwekeza, kujenga, kuendesha na kusimamia huduma ya Fiber-to-the-Home (FTTH).Upatikanaji bora wa huduma za intaneti unatarajiwa kuchochea ubunifu, ujasiriamali, elimu ya kidigitali, huduma za serikali mtandao (e-Government) na utoaji wa huduma za afya za kisasa, huku ukiimarisha zaidi mvuto wa Zanzibar kama kitovu cha uwekezaji, utalii na biashara katika ukanda huu.

Serikali ya Zanzibar kupitia Shirika la Mawasiliano Zanzibar (ZICTIA) itatoa ushirikiano katika masuala ya upatikanaji wa maeneo ya utekelezaji, uratibu wa kikanuni na usimamizi wa mradi ili kuhakikisha utekelezaji wake unafanikiwa.Mbali na uwekezaji wa miundombinu, ushirikiano huo pia utachangia maendeleo ya ujuzi wa kidigitali, uhamishaji wa maarifa na kujenga uwezo wa wataalamu wa ndani, hatua itakayosaidia kuandaa kizazi kijacho kushindana katika uchumi unaoendeshwa na teknolojia na kuunga mkono maono ya muda mrefu ya Zanzibar ya kuwa kitovu kinachoongoza kwa uchumi wa kidigitali Afrika Mashariki.

Akizungumza wakati wa hafla ya utiaji saini huo, Waziri wa Mawasiliano, Teknolojia ya Habari na Ubunifu Zanzibar, Mudrik Ramadhan Soraga, alisema ushirikiano huo ni sehemu ya jitihada za Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kuhakikisha wananchi wengi zaidi wanapata huduma bora za mawasiliano na kushiriki kikamilifu katika uchumi wa kidijitali.

Alisema tayari utekelezaji wa mradi huo umeanza kabla hata ya kutiwa saini kwa makubaliano hayo, jambo linalodhihirisha dhamira ya dhati ya pande zote mbili katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma hizo kwa haraka.











Na Mwandishi Wetu

WAFUGAJI nchini wamefurahishwa na mpango wa matumizi ya Mfumo wa Stakabadhi za Ghala kwenye sekta ya mifugo wakidai kuwa utaleta manufaa makubwa katika masoko na biashara shindani ya mifugo.

Akizungumza baada ya kutembelea banda la Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) katika Maonesho ya Mifugo na Mnada wa Kimataifa yanayofanyika katika Shamba la Mbogo, Chalinze mkoani Pwani, Mwenyekiti wa Chama Cha Wafugaji Tanzania (CCWT), Mrida Mshota, amesema mfumo huo utasaidia kutatua changamoto ya masoko ya mifugo nchini.

Amesema kupitia mpango huo wafugaji watapata fursa ya kujitangaza katika masoko ya kimataifa na kuuza mifugo yao kwa uhakika zaidi.

“Ukiwa na shamba lako na likasajiliwa na serikali sasa unakuwa na uhakika wa kuuza mifugo kwenye masoko makubwa ya kimataifa. Mpango huu ni mzuri na naiomba serikali iweke mkazo mkubwa kuhakikisha unaanza kutekelezwa haraka. Waziri Mkuu tayari alishasema jambo hili lishughulikiwe kwa haraka ili liwe na tija kwa wafugaji,” amesema Mshota.

Aidha, ameishauri Wizara ya Viwanda na Biashara kuweka mikakati madhubuti katika maeneo mbalimbali nchini ili utekelezaji wa mfumo huo uanze kabla ya mwaka huu kuisha.

“Sisi tuna kanda nane, hivyo tukitumia vizuri kanda zote serikali itakwenda kukusanya mapato bila kutumia nguvu kubwa. Kwa sasa utoroshaji wa mifugo ni mkubwa kwani baadhi ya wafugaji wanapeleka mifugo nje ya nchi bila utaratibu rasmi, lakini tukianza kutumia mfumo huu wenye masoko ya uhakika, tatizo hilo litapungua kwa kiasi kikubwa,” amesema.

Naye, Afisa Ubora wa WRRB, Bw. Anatolius Kabyemera, amesema mfumo huo utaleta uwazi katika biashara ya mazao na mifugo, kuongeza ushindani wa bei na kuhakikisha wafugaji pamoja na wakulima wanapata thamani halisi ya bidhaa zao.
Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima (TEWW) imeeleza kuwa ina mchango mkubwa katika kuwawezesha watoto, vijana na watu wazima waliokosa fursa ya elimu ndani ya mfumo rasmi kurejea na kuendelea na masomo yao.

Hayo yameelezwa na Mkuu wa Taasisi hiyo, Profesa Philipo Sanga, wakati akizungumza na waandishi wa habari Jijini Dodoma Juni 22, 2026, kwenye maadhimisho ya Wiki ya utumishi wa Umma.

Ameeleza majukumu makubwa ya TEWW ni kushughulikia elimu ya watu wazima na elimu nje ya mfumo rasmi, sekta ambayo imekuwa muhimu katika kuwasaidia wananchi wengi kupata elimu na ujuzi unaohitajika katika maisha na maendeleo ya taifa.

Amesema takwimu zinaonyesha kuwa kati ya kila watoto 10 kwa baadhi ya maeneo, watoto wanne hawapati fursa ya kuanza shule, huku kundi kubwa la wanafunzi likikatisha masomo katika ngazi mbalimbali za elimu.

“Katika kila wanafunzi 100, takribani 31 hudondoka na kushindwa kuendelea na masomo kwa ujumla, zaidi ya wanafunzi laki nne kutoka shule za msingi na sekondari hudondoka kila mwaka na kukosa fursa ya kuendelea na elimu."

Amebainisha kuwa bila uwepo wa Taasis ya Elimu ya Watu Wazima, idadi kubwa ya wananchi wengi wangeshindwa kupata nafasi ya kurejea katika mfumo wa elimu na kufikia malengo yao.

Kwa mujibu wa Profesa Sanga, Taasisi hiyo inatekeleza miradi mbalimbali ya elimu ya msingi na sekondari nje ya mfumo rasmi, inayolenga kuwapa wananchi fursa ya kupata elimu, maarifa na ujuzi unaowawezesha kujitegemea na kuchangia maendeleo ya taifa.

Aidha, amesema TEWW kupitia Chuo cha Elimu ya Juu cha Elimu ya Watu Wazima hutoa programu za elimu kuanzia ngazi ya cheti, stashahada, shahada hadi shahada za uzamivu kwa lengo la kuandaa wataalamu wabobevu watakaosaidia maendeleo ya nchi.

Ameongeza kuwa katika kila mkoa kuna viongozi wa elimu ya watu wazima wanaosimamia shughuli za taasisi hiyo na kuhakikisha huduma zinawafikia wananchi katika maeneo mbalimbali.

Aidha ameeleza changamoto mbalimbali zinazowakabili wanafunzi ndiyo chanzo kikuu cha kudondoka kwao kielimu, hivyo taasisi hiyo imejikita katika kuwasaidia kurejea masomoni na kutimiza ndoto zao za elimu.

Kwa upande wa elimu ya juu, Profesa Sanga amesema Taasis ya Elimu ya Watu Wazima imefanikiwa kudahili zaidi ya wanafunzi 6,000 na kwamba zaidi ya wanafunzi 2,000 huhitimu kila mwaka, jambo linaloonyesha mchango mkubwa wa taasisi hiyo katika kuboresha sekta ya elimu nchini.

Profesa Sanga amesema kupitia banda la TEWW katika Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea Jijini Dodoma hadi Juni 23, wananchi wanaweza kupata huduma mbalimbali ikiwemo taarifa za udahili na matumizi ya mfumo wa kutunza takwimu za elimu nje ya mfumo rasmi.


Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma 

NAIBU Waziri wa Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Regina Ndege Qwaray, amesema lengo la Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) ni kuwawezesha wananchi wanaoishi katika mazingira magumu na kaya maskini kujikwamua kiuchumi, kufikia ndoto zao na kuboresha maisha yao kwa kujitegemea.

Regina ametoa kauli hiyo leo alipokuwa akitembelea banda la TASAF katika Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika viwanja vya Chinangali Park jijini Dodoma.

Amesema TASAF imeendelea kufanya kazi kubwa ya kuelimisha wananchi kuhusu fursa mbalimbali zinazotolewa na mfuko huo, hatua ambayo imeongeza uelewa kwa kaya maskini na kuwasaidia kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo.

"Nawapongeza TASAF kwa kazi nzuri mnayoifanya. Msichoke kuendelea kumsaidia Mheshimiwa Rais katika kutekeleza majukumu ya kuwainua wananchi kiuchumi na kuifanya Tanzania kuwa imara kwa kuwawezesha watu kujitegemea badala ya kutegemea misaada," amesema Regina.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Singida, Halima Dendego, ameipongeza TASAF kwa kuendelea kutoa msaada wa elimu kwa watoto kutoka katika kaya maskini, jambo ambalo limechangia kuwawezesha kuendelea na masomo yao huku familia zao zikipata nafuu ya changamoto za kiuchumi.

Amesema uwekezaji katika elimu kupitia TASAF umekuwa na mchango mkubwa katika kujenga mustakabali bora wa watoto wanaotoka katika mazingira yenye uhitaji mkubwa.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Pangani, Gift Msuya, amesema viongozi wa wilaya hukutana na watoto wengi wenye uwezo mkubwa wa kitaaluma lakini wanakabiliwa na changamoto za kifedha zinazowazuia kufikia malengo yao ya elimu.

Kutokana na hali hiyo, ameshauri TASAF kuangalia uwezekano wa kuwa na mfumo utakaotambua kaya zenye uhitaji kupitia mamlaka za serikali za mitaa, ikiwemo zile zilizopo maeneo ya mijini ambazo mara nyingi hushindwa kuingia kwenye mifumo ya TASAF kupitia utaratibu wa kawaida wa usajili.

"Tuna kaya nyingi zenye uhitaji mkubwa mijini ambazo hazijafikiwa na programu za TASAF. Ni muhimu kuangalia namna ya kuzitambua na kuzifikia ili nazo zipate fursa ya kunufaika na huduma hizi," amesema Msuya.

Aidha, ameomba TASAF kuzingatia zaidi kaya zenye watoto yatima waliofiwa na wazazi wao, ili waweze kupata msaada unaohitajika na kuendelea na masomo pamoja na maisha yao ya kila siku bila vikwazo vikubwa vya kiuchumi.

Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yameendelea kuwa jukwaa muhimu kwa taasisi mbalimbali za serikali kuonyesha huduma wanazotoa kwa wananchi pamoja na mafanikio yaliyopatikana katika kuboresha ustawi wa jamii.




 


Na Janeth Raphael MichuziTv - Bungeni Dodoma

Mbunge wa Kigoma Mjini Clayton Revocatus Chipando (Baba levo) ameishauri Serikali na Bunge kufanya mapitio ya mfumo wa utozaji tozo katika sekta ya bodaboda, akisisitiza kuwa kundi hilo kubwa la vijana haliwezi kubebeshwa mzigo mpya wa kodi kutokana na hali yao ya kiuchumi.

Akichangia mjadala wa bajeti kuu ya Serikali, Chipando amesema bodaboda ni moja ya sekta zinazowezesha maisha ya mamilioni ya Watanzania, na kuongeza gharama mpya kutawaumiza zaidi wananchi walioko katika kipato cha chini.

Ameeleza kuwa takribani asilimia 75 ya waendesha bodaboda nchini ni vijana waliomaliza elimu ya msingi, hususan darasa la saba, ambao hawakuweza kuingia katika ajira rasmi, hivyo kujikuta wakijiajiri kwenye sekta isiyo rasmi ili kujikimu kimaisha.

Amesema badala ya kuongeza tozo katika sekta hiyo, Serikali inapaswa kutafuta vyanzo vingine vya mapato visivyoathiri moja kwa moja wananchi wenye kipato kidogo, huku akilinganisha hali hiyo na ongezeko la gharama katika bidhaa nyingine ambazo hazina athari kubwa kwa kundi hilo.

Katika hoja nyingine, mbunge huyo ameitaka Serikali kuwekeza zaidi kwenye teknolojia ya kisasa katika sekta ya ulinzi, ikiwemo matumizi ya ndege zisizo na rubani (drone) na vifaa vya kisasa vya kijeshi, ili kuendana na mabadiliko ya vita vya kisasa duniani, akitolea mfano wa migogoro kama ya Ukraine.

Aidha, katika sekta ya michezo na sanaa, Chipando amependekeza taasisi za kifedha kuwapa wasanii muda wa kutosha wa kurejesha mikopo wanayopewa kupitia programu za Serikali. Ameomba muda wa angalau miezi mitatu hadi sita ili kuwapa nafasi ya kurejesha mikopo baada ya kazi zao kuanza kuleta kipato.

Pia amesisitiza kuwa mikopo hiyo, ambayo hutolewa kupitia Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Samia Suluhu Hassan, inapaswa kuwa na masharti rafiki yanayolenga kuwawezesha walengwa kunufaika badala ya kubanwa na ratiba ngumu za marejesho.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza jambo na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Namibia Mhe. Dkt, Netumbo Nandi-Ndaitwah baada ya Rais huyo wa Namibia kuhitimisha Ziara yake ya Kitaifa ya siku 4 katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 22 Juni, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa amesimama na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Namibia Mhe. Dkt. Netumbo Nandi-Ndaitwah wakati wakipokea heshima ya Wimbo wa Taifa katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam kabla ya Rais huyo wa Namibia kuhitimisha Ziara yake ya Kitaifa ya siku 4 nchini Tanzania, tarehe 22 Juni, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza jambo na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Namibia Mhe. Dkt, Netumbo Nandi-Ndaitwah baada ya Rais huyo wa Namibia kuhitimisha Ziara yake ya Kitaifa ya siku 4 katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 22 Juni, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiagana na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Namibia Mhe. Dkt, Netumbo Nandi-Ndaitwah katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 22 Juni, 2026. Rais Mhe. Dkt. Ndaitwah amehitimisha Ziara yake ya Kitaifa ya siku 4 nchini Tanzania ambapo pamoja na kufanya mazungumzo na Rais Mhe. Dkt. Samia pia alitembelea Kambi ya Kihistoria ya Wapigania Uhuru wa nchi yake, Kongwa mkoani Dodoma.


atukio mbalimbali wakati Rais wa Jamhuri ya Namibia Mhe. Dkt, Netumbo Nandi-Ndaitwah akihitimisha Ziara yake ya Kitaifa ya siku 4 nchini Tanzania, katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 22 Juni, 2026.


Top News