Na Mwandishi Wetu

Dar es Salaam. Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imeendelea kutumia Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara (Sabasaba) kutoa elimu kwa wananchi kuhusu majukumu yake, huduma mbalimbali na umuhimu wa ithibati katika kuimarisha taaluma ya uandishi wa habari nchini.

Hatua hiyo imejidhihirisha leo baada ya Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa JAB, Wakili Patrick Kipangula, kuungana na maafisa wa Bodi katika banda la JAB lililopo Kijiji cha Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, kutoa elimu kwa wananchi, kujibu maswali mbalimbali na kuzungumza na waandishi wa habari waliotembelea banda hilo.

Akizungumza katika maonesho hayo, Wakili Kipangula alisema JAB imejipanga kuhakikisha wananchi na wadau wa sekta ya habari wanapata uelewa sahihi kuhusu majukumu ya Bodi pamoja na huduma zinazotolewa kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari.

Alisema ushiriki wa JAB katika maonesho ya Sabasaba unalenga kusogeza huduma karibu na wananchi, kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa ithibati kwa waandishi wa habari na kuhamasisha uzingatiaji wa maadili, weledi na uwajibikaji katika taaluma ya uandishi wa habari.

Mbali na kutoa elimu, JAB inaendelea kutoa huduma mbalimbali katika banda lake ikiwemo usajili wa waandishi wa habari, utoaji wa vitambulisho vya ithibati kwa waliokidhi vigezo, marekebisho ya taarifa za usajili pamoja na ushauri kuhusu huduma zinazotolewa na Bodi.

JAB imewahimiza waandishi wa habari, wadau wa sekta hiyo na wananchi kwa ujumla kutumia fursa ya Maonesho ya Sabasaba kutembelea banda lake ili kupata huduma, elimu na ufafanuzi kuhusu shughuli zake, huku ikisisitiza kuwa ithibati ni nyenzo muhimu katika kujenga taaluma ya uandishi wa habari yenye weledi, uwajibikaji na kuaminika.

Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa SGA Tanzania, Oscar Mgaya akizungumza wakati wa hafla hiyo.

Naibu Kamishna wa Polisi (DCP) Ulrich Matei (kushoto) akikabidhi zawadi Kwa John Amon ambaye ni mmoja wa wastaafu wa SGA Tanzania.
Naibu Kamishna wa Polisi (DCP) Ulrich Matei (wa pili kushoto) akisaidiana na wanachama wa Club 20 wa SGA kukata keki wakati wa shughuli ya kuwaaga wafanyakazi waliostaafu na kuwatambua wafanyakazi walihudumia kampuni hiyo kwa zaidi ya miaka 20. 

JESHI la Polisi limetoa wito wa ushirikiano wa karibu kati ya polisi na makampuni binafsi ya ulinzi kwa lengo la kupunguza matukio ya uhalifu pamoja na kudumisha amani nchini.

Wito huo umetolewa hivi karibuni na Naibu Kamishna wa Jeshi la Polisi (DCP) Ulrich Matei wakati wa hafla maalum iliyoandaliwa na kampuni ya ulinzi ya SGA Tanzania iliyolenga kuwaaga watumishi wa kampuni hiyo waliosataafu na kuwatambua wafanyakazi walioitumikia kampuni hiyo Kwa zaidi ya miaka 20.

baada ya kutumikia kampuni hiyo kwa zaidi ya miaka 20 kupitia programu inayojulikana kama Club 20.

Hafla hiyo ilifanyikia katika Bustani ya Hekima jijini Dar es Salaam na kuhudhuriwa na wawakilishi mbalimbali kutoka Jeshi la Polisi, Baraza la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA), uongozi na wafanyakazi wa kampuni ya SGA pamoja na wageni wengine waalikwa.

Alisema kuwa sekta binafsi katika sekta ya ulinzi pia ina jukumu la kuhakikisha nchi inakuwa salama amapo alitoa wito kwa wastaafu walioagwa kuendelea kutoa michango na uzoefu wao ili amani iliyoko hapa nchini iendelee kutamalaki.

DCP Matei aliupongeza uongozi wa SGA kwa kuendelea kuthamini michango inayotolewa na wafanyakazi wake sambamba na kuhakikisha ustawi wa watumishi wa kampuni hiyo ikiwemo kuendelea kuwajengea uwezo.

”Makampuni mengi huwa hayazingatii maagizo yanayoelekeza makampuni binafsi ya ulinzi kuendelea kuwajengea mazingira mazuri ya kiutendaji watumishi wao kupitia mafunzo, uhakiki, usimamizi na maboresho ya mishahara; kwa SGA niwapongeze kwa kujitahidi kutekeleza maagizo haya, nyinyi ni mfano mzuri wa kuigwa na makampuni mengine”, alisema.

Aidha alitoa pongezi kwa uongozi wa kampuni hiyo kwa kuwa na utaratibu wa kuwapongeza wafanyakazi waliofanya kazi kwa zaidi ya miaka 20 na kuongeza kwamba kwa watumishi zaidi ya 95 kufanya kazi kwa zaidi ya miaka 20 ni jambo linalostahili kusherehekewa na kupongezwa.

Alitoa wito kwa makampuni yote ya ulinzi ya binafsi kuongeza ufanisi na kuwekeza zaidi katika teknolojia, mafunzo kwa watumishi wao, kufuata sheria na kuzingatia haki za binadamu ili kupunguza malalamiko wakati wa utoaji wa huduma.

DCP Matei aliahidi kuwa Jeshi la Polisi litaendelea kutoa ushirikiano wake wa dhati kwa makampuni binafsi jambo ambalo amesema ni muendelezo wa ushirikiano huo kwa miaka mingi iliyopita.

Akizungumza kwa niaba ya SGA Tanzania, Mkuu wa kitengo cha fedha cha kampuni hiyo Bw. Jonathan Geleta, aliushukuru uongozi wa Jeshi la Polisi kwa ushirikiano ambao jeshi hilo limetoa na linaendelea kutoa kwa makampuni binafsi ya ulinzi hapa nchini.

"Nichukue fursa hii kwa niaba ya uongozi wa SGA kuahidi kuwa kampuni yetu itaendelea kufuata miongozo na kanuni zote kama zinavyotolewa na Jeshi la Polisi ili kuhakikisha ufanisi katika kutoa huduma zetu ndani ya jamii”, alisema.

Aliwapongeza wastaafu kwa huduma yao bora waliyotoa wakati wakiitumikia kampuni hiyo, ambapo alitoa rai kwa wastaafu hao kuwa mabalozi wazuri wa kuhimiza amani wakati wakianza maisha mapya ndani ya jamii.

SGA Security ni kampuni ya kwanza ya ulinzi ya kibinafsi nchini Tanzania, iliyoanza kufanya shughuli zake rasmi hapa nchini miaka 42 iliyopita, ambapo kwa sasa inaajiri zaidi ya Watanzania 5,000 katika mtandao wake ulioenea hapa nchini.

Pamoja na huduma nyingine bora, kampuni hiyo pia inatoa huduma bora zaidi ya usafirishaji wa bidhaa zikiwemo zile zenye thamani kubwa kwa usalama wa hali ya juu na uhakika.

SGA pia inatoa huduma za ulinzi wa hali ya juu, huduma za dharura pamoja na vifaa vya usalama wa kielektroniki ambavyo husaidia kuhakikisha usalama wa wateja wake, ambapo kutokana na huduma hizo bora kampuni hiyo imepata tuzo mbalimbali za ndani na nje ya nchi.
Na. Mwandishi Wetu - Arusha

Tanzania ipo tayari kwa mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON 2027) ikiwa mwenyeji kwa kushirikiana na Kenya na Uganda ambapo maandalizi yamefikia hatua nzuri kwa kuzingatia viwango vya Shirikisho la Mpira wa Miguu Barani Afrika (CAF) vinavyotakiwa.

Akizungumza hii leo Julai 3, 2026 Jijini Arusha kwa niaba ya Mwenyekiti wa Kamati ya Kitaifa ya Makatibu Wakuu ya Maandalizi ya Michuano hiyo, Dkt. Jim Yonazi, Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii Dkt. Hassan Abbasi amesema Serikali imejipanga kikamilifu kuhakikisha michuano hiyo inafana kwa kuzingatia mipango na mikakati thabiti iliyopo.

Dkt. Abbasi ameiongoza Kamati hiyo iliyotembelea viwanja vitakavyotumika wakati wa michuano hiyo ikiwemo Kiwanja cha Mazoezi cha Mgambo, kiwanja cha mazoezi cha Engutoto, Kiwanja cha mazoezi Magereza, uwanja Mpya wa Arusha pamoja na ukaguzi wa barabara za mjini zinazosimamiwa na Wakala wa Barabara Tanzania-TANROADS pamoja na zinasosimamiwa na Wakala wa Barabara za mjini na vijijni -TARURA zitakazoingia na Kutoka Katika uwanja wa Arusha, kujionea maendeleo ya ukarabati na maboresho mbalimbali kuelekea michuano hiyo.

Aidha amesema kuwa, michuano hiyo itakuwa ya kihistoria kwa kukutanisha na kuvutia mamilioni ya watu barani Afrika na duniani kote, ambapo ni kwa mara ya kwanza mashindano hayo kuandaliwa kwa pamoja na Mataifa matatu ya Afrika Mashariki.

Aliongezea kuwa, Tanzania imejipanga kupokea Maelfu ya mashabiki, wachezaji, na viongozi wa soka wanatarajiwa kukusanyika na kuleta mwamko mkubwa kupitia Mashindano Makubwa ya Kombe la Mataifa Afrika (AFCON 2027).

"Ni wakati wetu sasa, kuipa nchi heshima yake kuelekea Michuano hiyo ya AFCON, kila mmoja akae tayari katika eneo lake na kujua kuwa anajukumu la kuifanikisha michuano hii na kwa viwango vya kimataifa," alisema Dkt. Abbasi.

Pia alisisistiza Wakandarasi kwenye miradi mbalimbali ya kuboresha miundombinu kuongeza kasi ili kumaliza kazi hizo kwa wakati bila kukwamisha maandalizi hayo.

Kwa upande wake Katibu Tawala wa Mkoa wa Arusha Dkt. Toba Nguvila amesema kuwa mkoa umeendelea na maandalizi yote muhimu ikiwemo ya ukarabati wa miundombinu itakayotumika, kuhakikisha upatikanaji wa huduma za maji, kuboresha maeneo ya utoaji wa huduma za kiafya ikiwemo hospitali, masuala ya mawasiliano, pamoja na umeme na kuhakikisha vinapatikana kwa ubora na viwango.

“Jiji linaimarisha miundombinu ya barabara, huku kukiwa na ujenzi na ukarabati wa hoteli za kutosha zitakazotoa huduma pamoja na uboreshwaji wa vituo vya afya vya kutolea huduma za afya ikiwemo hospitali ya Mount Meru, JKCI pamoja na NSK ambazo zitatoa huduma za kiafya kwa ubora na viwango,” alisema Dkt. Nguvila.












Mkurugenzi wa Taasisi ya Tiba ya Mifupa na Ubongo Muhimbili (MOI), Balozi Dk. Mpoki Ulisubisya (wa pili kushoto), akipata maelezo kutoka kwa Meneja wa Kitengo cha Uchunguzi wa saratani na elimu kwa umma wa Taasisi ya Saratani Ocean Road, Dk. Maguha Stephano, alipotembelea banda la taasisi hiyo katika Maonesho ya Kimataifa ya 50 ya Biashara, Dar es Salaam.

Taasisi ya Saratani Ocean Road imewataka Watanzania wanaotembelea Maonesho ya Kimataifa ya 50 ya Biashara 'Saba Saba' kujitokeza katika banda la taasisi hiyo kupata elimu na huduma za uchunguzi wa saratani bila malipo.

Akizungumza katika maonesho hayo, Meneja wa Kitengo cha Uchunguzi wa saratani na elimu kwa umma wa Taasisi ya Saratani Ocean Road, Dk. Maguha Stephano, amesema taasisi hiyo imeweka kambi maalumu kwa kipindi chote cha maonesho kwa lengo la kuwafikia wananchi wengi zaidi kupitia huduma za kinga, elimu na uchunguzi wa mapema wa saratani.

Amesema huduma zinazotolewa ni elimu kuhusu ugonjwa wa saratani, Lishe,vichochezi na visababishi vyake pamoja na namna wananchi wanavyoweza kujikinga na kushiriki katika mapambano dhidi ya ugonjwa huo.

"Mbali na elimu, tunatoa huduma za uchunguzi wa saratani bure kwa wananchi wote watakaofika kwenye banda letu," amesema Dk. Maguha.

Amesema kwa upande wa saratani ya matiti, wanawake wa umri wote wanakaribishwa kufanyiwa uchunguzi huku wakipatiwa mafunzo ya namna ya kujichunguza wenyewe majumbani kubaini dalili za awali.

Dk. Maguha amesema ugonjwa wa saratani ya mlango wa kizazi, unaendelea kuwa miongoni mwa changamoto kubwa za afya nchini.

Pia amesema maambukizi ya virusi vya Human Papilloma Virus (HPV) ndiyo chanzo kikuu cha ugonjwa huo, huku takribani asilimia 90 ya visa vya saratani ya mlango wa kizazi vikihusishwa na maambukizi hayo.

Amesema njia muhimu za kupambana na ugonjwa huo ni kuwapatia mabinti miaka 9-14 chanjo ya HPV na kuwahamasisha wanawake walioanza kujamiiana pamoja na walioko kwenye makundi ya hatari kujitokeza kwa uchunguzi wa mapema ili kubaini mabadiliko kabla hayajawa saratani.

Aidha, amesema taasisi hiyo inatoa huduma za uchunguzi wa saratani ya tezi dume kwa wanaume, hasa wenye umri wa miaka 50 na kuendelea, kutokana na kuongezeka kwa hatari ya kupata ugonjwa huo kadiri umri unavyoongezeka.

Amesema uchunguzi huo hufanyika kwa njia rahisi ya kipimo cha damu kinachochukuliwa kwenye kidole Kama kipimo cha Malaria, huku majibu yakipatikana ndani ya dakika chache na mgonjwa kupatiwa ushauri wa kitaalamu kulingana na matokeo yake.

Dk. Maguha amewahimiza Watanzania wote wanaotembelea Maonesho ya Saba Saba kutembelea banda la Taasisi ya Saratani Ocean Road ili kunufaika na huduma hizo.





BODI ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA) inashiriki Maonesho ya Kimataifa ya Biashara ya 50 yanayoendelea kwenye Viwanja vya Sabasaba jijini Dar es Salaam, ikiwa ni jitihada za kuonyesha huduma mbalimbali zinazotolewa na Bodi hiyo pamoja na kutoa elimu kwa wananchi.

Banda la NBAA lipo ndani ya jengo la Wizara ya Fedha linawahudumia wananchi kwa kutoa maelekezo ya usajili wa mitihani katika ngazi mbalimbali za Taaluma ya Uhasibu, pamoja na kutoa maelekezo kuhusu ulipaji wa ada na huduma nyingine muhimu.

Katika kipindi hiki cha Sabasaba Bodi imewasogezea wananchi huduma karibu kwa kutoa huduma zote kama vile usajili wa watahiniwa wa mitihani ya Bodi, usajili wa wanachama wa ngazi mbalimbali, usajili wa Makampuni, usajili wa kozi mbalimbali zinazoendeshwa na Bodi.

Aidha, NBAA kwa sasa inatumia mifumo ya kidijitali kutoa huduma zake, ambapo wananchi wanaweza kufikia huduma hizo kupitia tovuti rasmi ya Bodi ambayo ni www.nbaa.go.tz.

Maonesho haya ya Sabasaba ni fursa kubwa kwa Bodi ya NBAA kuwasiliana moja kwa moja na wananchi na wadau mbalimbali wa taaluma ya uhasibu na ukaguzi, ili kuboresha utoaji wa huduma na kuelimisha kuhusu umuhimu wa taaluma hiyo katika maendeleo ya taifa.
Wafanyakazi wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA) wakiwa kwenye picha ya pamoja katika banda la Bodi hiyo lililopo ndani ya jengo la Wizara ya Fedha.
Huduma zikiendelea kwenye banda la NBAA
TANZANIA imeendelea kupiga hatua katika sekta ya afya baada ya kuanza kutumika kwa kipimo kipya cha Checkfor UTI Test, kinachomwezesha mtu kujipima akiwa nyumbani ili kubaini uwezekano wa maambukizi ya njia ya mkojo (UTI).

Akizungumza hivi karibuni jijini Dar es Salaam, Dkt. Eshton Nkala alisema maambukizi ya UTI ni miongoni mwa changamoto za kiafya zinazowakumba watu wengi, huku dalili zake zikijumuisha kukojoa mara kwa mara, maumivu au muwasho wakati wa kukojoa, maumivu ya chini ya tumbo na mkojo kubadilika rangi au kuwa na harufu isiyo ya kawaida.

Alisema changamoto kubwa imekuwa ni kuchelewa kutambua dalili na kufika katika vituo vya afya, wakati utambuzi wa mapema husaidia kupunguza uwezekano wa maambukizi kuongezeka, kujirudia au kusababisha madhara zaidi kiafya.

Kwa mujibu wake, Checkfor UTI Test humsaidia mtu kupata taarifa za awali kuhusu uwezekano wa kuwa na UTI akiwa nyumbani, lakini hakichukui nafasi ya daktari wala hospitali, bali humwezesha mtumiaji kuchukua hatua mapema na kufika kituo cha afya kwa ushauri wa kitaalamu, vipimo zaidi na matibabu stahiki.

Dkt. Nkala alisema kipimo hicho kinazalishwa nchini na kampuni ya Canadian Biotech, hatua inayoonyesha mchango wa viwanda vya ndani katika uzalishaji wa vifaa tiba vinavyosaidia jamii kujitambua mapema na kuchukua hatua kwa wakati.

Aliongeza kuwa Checkfor UTI Test kinapatikana kupitia JD Pharmacy, Bariki Pharmacy na Cugra General Supplier, huku akisisitiza kuwa wananchi hawapaswi kupuuza dalili za UTI, bali wajitambue mapema na kutafuta matibabu sahihi kwa wakati.


Na Karama Kenyunko Michuzi Tv
MWENYEKITI wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Tundu Lissu ameiomba Mahakama ya Rufani kutupilia mbali maombi ya marejeo yaliyowasilishwa na Mkurugenzi wa Mashtaka nchini (DPP), akidai hayana msingi wa kisheria na yanalenga kuchelewesha usikilizwaji wa kesi ya tuhuma za uhaini inayomkabili.

Lissu alidai hayo mbele ya jopo la majaji watatu wa Mahakama ya Rufani baada ya Jamhuri kufungua shauri la mapitio kupinga uamuzi wa Mahakama Kuu uliotupilia mbali notisi ya Jamhuri ya kuwasilisha ushahidi mpya katika kesi hiyo.

Alidai uamuzi wa Mahakama Kuu wa Februari 24, 2026 haukumaliza kesi ya msingi ya uhaini, hivyo ni uamuzi mdogo usioruhusiwa kukatiwa rufaa wala kuwasilishwa maombi ya marejeo kwa mujibu wa Sheria ya Mamlaka ya Rufani.

Lissu pia alidai DPP hakupaswa kuwasilisha maombi hayo moja kwa moja Mahakama ya Rufani bali alitakiwa kwanza kuandika barua rasmi kwa Jaji Mkuu.

Kwa upande wa Jamhuri, Wakili wa Serikali Mkuu Nassoro Katuga na Job Mrema waliieleza Mahakama kuwa Lissu ametegemea kanuni za mashauri ya madai badala ya jinai na kwamba maombi ya DPP yamewasilishwa kwa mujibu wa Sheria ya Mahakama ya Rufani na Kanuni zake.

Katuga alidai Mahakama Kuu ilikataa ushahidi huo kabla haujapokelewa na kupimwa, jambo ambalo lilinyima Jamhuri haki ya kusikilizwa kikamilifu, huku akisisitiza kuwa Mahakama ilipaswa kuangalia uhalali wa notisi ya kuongeza ushahidi.

Mrema naye alidai pingamizi la awali la Lissu halina uwezo wa kuondoa shauri lote na kwamba halijazingatia sheria ya sasa kwa kuwa linahusu mashauri ya madai.

Katika majibu yake, Lissu aliiomba Mahakama itupilie mbali maombi hayo na iamuru DPP amlipe fidia kwa kile alichodai ni ucheleweshaji wa makusudi wa shauri lake, akisema amekaa gerezani kwa mwaka mmoja na miezi mitatu huku kesi ikicheleweshwa kwa siku 139.

Katuga alipinga madai hayo akieleza kuwa maombi hayo hayajalenga kuchelewesha kesi na kwamba Mahakama ya Rufani ina mamlaka ya kuhakikisha mwenendo wa Mahakama Kuu unafuata sheria.

Baada ya kusikiliza hoja za pande zote, Mahakama iliahirisha shauri hilo hadi itakapotoa uamuzi wake kwa tarehe ambayo pande zote zitajulishwa.




Waziri wa Fedha Balozi Khamis Mussa Omary akipata maelezo kutoka kwa Mtakwimu Mkuu wa Serikali, Dkt. Amina Msengwa wakato alipotembelea katika Banda la Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) wakati alipotembelea banda hilo katika maonesho ya 50 ya Biashara Kimataifa yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere (Sabasaba) jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Fedha Balozi Khamis Mussa Omary akipata maelezo wakati Maktaba mtandao YA NBS jinsi inavyofanya kazi ambapo wadau mbalimbali wanaweza kupata machapisho ya Kitakwimu alipotembelea katika Banda la Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) kwenye maonesho ya 50 ya Biashara Kimataifa yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere (Sabasaba) jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Fedha Balozi Khamis Mussa Omary akizungumza katika Banda la Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) wakati alipotembelea banda hilo katika maonesho ya 50 ya Biashara Kimataifa yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere (Sabasaba) jijini Dar es Salaam.

Waziri wa Fedha Balozi Khamis Mussa Omary akipata maelezo kutoka kwa Kamishina wa Sensa ,Spika Mstaafu Anna Makinda wakati Waziri huyo alipotembelea katika Banda la Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) wakati alipotembelea banda hilo katika maonesho ya 50 ya Biashara Kimataifa yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere (Sabasaba) jijini Dar es Salaam.


Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

MIXX imewakutanisha wajasiriamali 18 katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba), ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuwawezesha kutangaza bidhaa na huduma zao pamoja na kupanua masoko.


Akizungumza katika maonesho hayo, Mkuu wa Kanda ya Kusini ya Dar es Salaam wa MIXX by YAS, Robert Kasulwa, alisema wajasiriamali hao ni wanufaika wa awamu ya pili ya mradi wa Anzia Ulipo, unaolenga kuwawezesha Watanzania kujikwamua kiuchumi kupitia ujasiriamali.

Kasulwa alisema katika awamu hiyo, jumla ya wajasiriamali 48 wamenufaika na mafunzo pamoja na uwezeshaji wa biashara, huku 18 kati yao wakipata nafasi ya kushiriki maonesho ya Sabasaba ili kutangaza bidhaa zao na kukutana na wateja pamoja na wadau mbalimbali wa biashara.

Alieleza kuwa lengo la mradi huo ni kuwafikia Watanzania wengi zaidi na kuwainua kiuchumi kwa kuwajengea uwezo wa kuanzisha na kukuza biashara endelevu katika maeneo mbalimbali nchini.

"MIXX by YAS inaendelea kushirikiana na wajasiriamali kwa kuwapa fursa za kujifunza, kuonyesha bidhaa zao na kupanua mtandao wa biashara. Tunaamini uwezeshaji huu utachochea ukuaji wa uchumi wa mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla," alisema Kasulwa.

Aliongeza kuwa kampuni hiyo itaendelea kutekeleza programu mbalimbali za uwezeshaji wa wananchi kwa lengo la kuongeza ushiriki wa Watanzania katika shughuli za kiuchumi na kutumia huduma za kifedha za kidijitali kukuza biashara zao.







Na Mwandishi Wetu - Dar es Salaam.


Kadri Maonesho ya 56 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba) yanavyoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania (TAEC) imeendelea kuthibitisha kuwa teknolojia ya nyuklia siyo teknolojia ya kutumika kwenye uzalishaji wa nishati pekee, bali ni nyenzo muhimu inayochochea maendeleo ya kiuchumi, biashara, uwekezaji na ustawi wa jamii kupitia matumizi yake katika sekta mbalimbali za maendeleo.

Leo ikiwa ni siku ya sita tangu kuanza kwa maonesho hayo yaliyofunguliwa rasmi tarehe 28 Juni na yanayotarajiwa kuhitimishwa tarehe 13 Julai 2026, banda la TAEC limeendelea kuwa moja ya maeneo yanayovutia idadi kubwa ya wananchi, wanafunzi, watafiti, wawekezaji, wafanyabiashara na wadau kutoka ndani na nje ya nchi wanaotaka kupata uelewa kuhusu nafasi ya teknolojia ya nyuklia katika maendeleo ya Tanzania.

Ushiriki wa TAEC katika maonesho haya unaendana na dhamira ya Serikali ya kuhakikisha wananchi wanapata elimu sahihi kuhusu matumizi salama ya mionzi na teknolojia ya nyuklia pamoja na mchango wake katika kukuza uchumi wa taifa kupitia uzalishaji wenye tija, huduma bora za afya, usalama wa chakula, maendeleo ya viwanda, utafiti na uhifadhi wa mazingira.

Akizungumza katika banda la TAEC lililopo ndani ya Banda Kubwa la China, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano wa TAEC, Bwana Peter Ngamilo, amesema maonesho ya Sabasaba ni jukwaa muhimu linaloiwezesha TAEC kuwasiliana moja kwa moja na wananchi na wadau mbalimbali, kuwaelimisha kuhusu majukumu ya Tume pamoja na fursa zinazotokana na matumizi ya teknolojia ya nyuklia katika maendeleo ya Taifa.

“Lengo letu kubwa ni kuhakikisha wananchi wanafahamu kuwa teknolojia ya nyuklia ni nyenzo muhimu ya maendeleo. Kupitia maonesho haya tunaendelea kutoa elimu kuhusu matumizi salama ya mionzi, wajibu wa TAEC katika usimamizi na udhibiti wa matumizi ya mionzi nchini, pamoja na namna teknolojia hii inavyochangia kukuza biashara, kuongeza tija katika uzalishaji na kuboresha maisha ya wananchi,” amesema Bwana Ngamilo.

Ameeleza kuwa wananchi wengi wamekuwa wakitembelea banda la TAEC kwa lengo la kupata ufafanuzi kuhusu teknolojia ya nyuklia na matumizi yake katika sekta mbalimbali, hali inayoonyesha kuwa uelewa wa jamii kuhusu teknolojia hiyo unaendelea kuongezeka siku hadi siku.

Katika sekta ya afya, TAEC imekuwa ikiendelea kutoa elimu kuhusu matumizi ya mionzi katika uchunguzi wa magonjwa, tiba ya saratani, tiba za nyuklia na uchunguzi wa kitaalamu unaowezesha madaktari kutoa huduma zenye usahihi zaidi kwa wagonjwa. Matumizi haya yameendelea kuboresha ubora wa huduma za afya nchini na kuongeza uwezo wa taasisi za tiba kutumia teknolojia za kisasa katika kuokoa maisha ya wananchi.

Kwa upande wa kilimo, wananchi wanaelimishwa namna teknolojia ya nyuklia inavyosaidia kuboresha mbegu za mazao, kuongeza uzalishaji, kudhibiti wadudu waharibifu wa mazao, kuhifadhi chakula baada ya kuvunwa na kuongeza usalama wa chakula. Teknolojia hizi zinachangia kuongeza ushindani wa bidhaa za kilimo katika masoko ya ndani na nje ya nchi.

Katika sekta ya mifugo, TAEC inaendelea kuhamasisha matumizi ya teknolojia ya nyuklia katika utambuzi wa magonjwa ya mifugo, kuboresha uzalishaji wa mifugo, kuimarisha lishe ya wanyama na kusaidia programu za uzalishaji zinazoongeza tija kwa wafugaji.

Sekta ya viwanda nayo ni miongoni mwa maeneo yanayonufaika kwa kiwango kikubwa kupitia matumizi ya teknolojia ya nyuklia. Kupitia teknolojia za mionzi, viwanda vinaweza kufanya ukaguzi wa ubora wa bidhaa bila kuziharibu (Non-Destructive Testing), kupima unene wa bidhaa mbalimbali, kufanya vipimo vya ubora wa miundombinu, kutambua hitilafu katika mitambo na kuongeza usalama wa uzalishaji. Teknolojia hizi husaidia kupunguza gharama za uzalishaji, kuongeza ubora wa bidhaa na kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania katika masoko ya kikanda na kimataifa.

Aidha, katika sekta ya nishati na utafiti, TAEC inaendelea kushirikiana na taasisi mbalimbali za kitaifa na kimataifa kujenga uwezo wa matumizi ya teknolojia za nyuklia katika tafiti zinazolenga kutatua changamoto za maendeleo, usimamizi wa rasilimali za maji, ulinzi wa mazingira na matumizi bora ya maliasili.

Kwa mujibu wa Bwana Ngamilo, elimu inayotolewa katika maonesho haya pia inalenga kuondoa dhana potofu ambazo baadhi ya wananchi wamekuwa nazo kuhusu teknolojia ya nyuklia.

“Wananchi wengi walikuwa wakihusisha teknolojia ya nyuklia na silaha pekee, lakini wanapofika katika banda letu wanajionea ushahidi kuwa teknolojia hii inagusa maisha yao ya kila siku kupitia huduma za afya, uzalishaji wa chakula, maendeleo ya viwanda, utafiti, usimamizi wa mazingira na sekta nyingine nyingi zinazochochea maendeleo ya uchumi wa Taifa.”

Maonesho ya Sabasaba yameendelea kuwa jukwaa muhimu la kuunganisha taasisi za Serikali, sekta binafsi, wawekezaji na wananchi katika kuonesha bidhaa, huduma na ubunifu unaochochea biashara na maendeleo ya uchumi wa Tanzania. Ushiriki wa TAEC katika maonesho hayo unaonesha dhamira ya Serikali ya kuhakikisha teknolojia ya nyuklia inatumika kwa amani, usalama na manufaa ya wananchi wote huku ikichangia utekelezaji wa dira ya maendeleo ya taifa kupitia sayansi, teknolojia na ubunifu.

TAEC inaendelea kuwakaribisha wananchi wote kutembelea banda lake lililopo ndani ya Banda Kubwa la China, Vyumba Na. 60 na 61, katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, Barabara ya Kilwa, Dar es Salaam, ili kujionea teknolojia mbalimbali zinazotumiwa nchini na kupata elimu kuhusu mchango wa teknolojia ya nyuklia katika kujenga uchumi imara, kuongeza ushindani wa biashara na kuharakisha maendeleo endelevu ya Tanzania.



Waziri wa Fedha Balozi Khamis Mussa Omary akipata maelezo katika Banda la Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA) wakati alipotembelea banda hilo katika maonesho ya 50 ya Biashara Kimataifa yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere (Sabasaba) jijini Dar es Salaam.

Waziri wa Fedha Balozi Khamis Mussa Omary akikabidhiwa mfuko uliowekewa taarifa mbalimbali za Taasisi  katika Banda la Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA) wakati alipotembelea banda hilo katika maonesho ya 50 ya Biashara Kimataifa yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere (Sabasaba) jijini Dar es Salaam.

Top News