Na Janeth Raphael MichuziTv -Bungeni Dodoma

Mbunge wa Kilolo, Ritha Kabati ameibua changamoto mbalimbali zinazokabili Wilaya ya Kilolo, akisisitiza kuwepo kwa mapungufu makubwa katika makazi ya askari, miundombinu ya vituo vya polisi pamoja na upungufu wa vifaa vya usafiri kwa askari kata, hali inayodaiwa kuathiri kasi ya utoaji wa huduma za kiusalama wilayani humo.

Akichangia mjadala wa makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa mwaka wa fedha 2026/27, Kabati amesema kuwa hali ya makazi ya askari bado si rafiki, kwani wengi wao hulazimika kuishi mbali na vituo vyao vya kazi. Amesema hali hiyo inasababisha kuchelewa kwa majibu ya haraka pindi matukio ya kiusalama yanapotokea, hivyo kuathiri ufanisi wa kazi za vyombo vya ulinzi na usalama.

Aidha, ameeleza kuwa katika Wilaya ya Kilolo hakuna mpango wa makazi ya askari uliotekelezwa kwa kiwango cha kuridhisha, jambo linalowafanya askari kuishi kwa mtawanyiko na kufanya kazi katika mazingira magumu yasiyo na uhakika wa ustawi wao.

Katika eneo la usafiri, Mbunge huyo amesema askari kata wanakabiliwa na uhaba mkubwa wa pikipiki, hali inayowafanya washindwe kufika kwa wakati katika maeneo ya matukio, hususan kutokana na ubovu wa baadhi ya barabara zinazotumika, ambazo mara nyingi haziwezi kupitika kwa urahisi.

Akiweka msisitizo wa kutafuta suluhisho la haraka, Kabati amesema yuko tayari kuanza kuchangia pikipiki kwa ajili ya askari hao ili kusaidia kuboresha utendaji kazi wao, endapo Serikali itashindwa kukidhi mahitaji hayo kwa wakati mmoja.

Katika hoja nyingine, amelitaja pia kituo cha polisi cha Ilula kuwa katika hali mbaya kutokana na uchakavu wa miundombinu yake, akiiomba Serikali kulipa kipaumbele kwa ajili ya ukarabati mkubwa au ujenzi mpya ili kuendana na mahitaji ya sasa ya huduma za ulinzi na usalama.

Mbunge huyo pia alipendekeza eneo la Igesa Mgagao, ambalo awali lilitumika kama kambi ya wapigania uhuru, liendelezwe na kuwekewa mkakati maalum wa kitalii ili liwe kivutio cha kihistoria cha taifa, akisema linaweza kuongeza fursa za utalii wa ndani endapo litaboreshwa ipasavyo.

Vilevile, alihoji Serikali kuhusu hatua iliyofikiwa katika mchakato wa kuwawekea utaratibu maalum Watanzania walioko nje ya mfumo rasmi wa uraia au wanaoishi nje ya nchi lakini wana mchango mkubwa kiuchumi kupitia uwekezaji na shughuli za uzalishaji, akisisitiza kuwa kundi hilo linaweza kuchangia kwa kiasi kikubwa katika ukuaji wa uchumi wa taifa endapo litapewa mfumo rasmi wa kisheria.

Aidha, Kabati ameitaka Serikali kufanya mapitio ya sheria na kanuni zinazosimamia utendaji wa vyombo vya ulinzi na usalama, akieleza kuwa baadhi ya sheria zimepitwa na wakati na zinahitaji maboresho ili kuongeza ufanisi, kuboresha ustawi wa watumishi na kuimarisha utoaji wa huduma kwa wananchi.

Kwa ujumla, mchango wa Mbunge Kabati umeibua kwa kina changamoto za kiusalama, miundombinu na kijamii zinazoikabili Wilaya ya Kilolo, huku akisisitiza umuhimu wa Serikali kuongeza uwekezaji katika makazi ya askari, vifaa vya usafiri, ukarabati wa vituo vya polisi pamoja na maboresho ya sheria ili kuimarisha utendaji wa vyombo vya ulinzi na usalama nchini.



Na Mwandishi Wetu.

Mikutano ya ngazi ya juu iliyohusisha makundi mbalimbali ya upinzani nchini Sudan Kusini imefanyika jijini Dar es Salaam tarehe 21 na 22 Mei, 2026 ikiwa ni sehemu ya juhudi mpya za kufufua mchakato wa amani jumuishi baada ya kusuasua kwa utekelezaji wa makubaliano ya amani ya mwaka 2018.

Mazungumzo hayo yaliongozwa na Rais wa Awamu ya Nne Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, ambaye ni Mwakilishi Maalum wa Umoja wa Afrika kwa Ukanda wa Pembe ya Afrika na Bahari ya Shamu.

Majukumu yake makuu yanajumuisha: Upatanishi wa Amani: Kusimamia diplomasia ya kuzuia migogoro na kuongoza mazungumzo jumuishi ili kutatua changamoto za kisiasa na kiusalama katika ukanda huo.

Ushirikiano wa Kikanda: Kufanya kazi kwa karibu na jumuiya na taasisi mbalimbali kama vile IGAD na Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) ili kujenga misingi thabiti ya amani na usalama.

Kwa ujumla, mikutano hiyo ilionyesha dhamira ya Umoja wa Afrika na wadau wa kikanda katika kuimarisha mazungumzo ya kisiasa na kuhakikisha mazingira ya amani na utulivu yanaimarishwa kuelekea uchaguzi mkuu baadaye mwaka huu nchini Sudan Kusini.

Mikutano hiyo pia ililenga kuisaidia Umoja wa Afrika kupata picha kamili ya hali ya kisiasa na kiusalama nchini Sudan Kusini kabla ya uchaguzi uliotarajiwa kufanyika baadaye mwaka huo wa 2026.

Pichani, Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Kikwete akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya wajumbe wa makundi yaliyoshiriki mikutano hiyo, yakiwemo United People’s Alliance (UPA), SSOMA, SPLM-IO, pamoja na People’s Coalition for Civil Action na Federal Democratic Party. Picha na Issa Michuzi
Na Karama Kenyunko, Michuzi TV


MAMLAKA ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imesema msimu wa Kipupwe wa Juni hadi Agosti (JJA) mwaka 2026 unatarajiwa kutawaliwa na hali ya baridi katika maeneo mengi ya nchi, huku mwezi Julai ukitajwa kuwa na vipindi vya baridi kali zaidi.

Akizungumza na waandishi wa habari wakati akitangaza utabiri huo, leo Mei 25, 2026 Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Nchini Dkt. Ladislaus Chang’a, amesema maeneo mbalimbali ya Tanzania yatashuhudia viwango tofauti vya hali ya joto, upepo pamoja na vipindi vya mvua nje ya msimu.

Dkt. Chang’a amesema hali ya baridi ya wastani hadi joto kiasi inatarajiwa katika Kanda ya Ziwa Victoria, Kanda ya Magharibi, Kanda ya Kusini, Nyanda za Juu Kusini-Magharibi pamoja na Mkoa wa Singida.

Aidha, maeneo ya Ukanda wa Pwani ya Kaskazini na maeneo ya nchi kavu, Nyanda za Juu Kaskazini-Mashariki, Ukanda wa Pwani ya Kusini pamoja na Mkoa wa Dodoma yanatarajiwa kuwa na hali ya joto kiasi hadi baridi ya wastani.

Mbali na hali ya baridi, Dkt. Chang’a amesema baadhi ya maeneo yatapata vipindi vya mvua nje ya msimu, hususan maeneo ya Ukanda wa Ziwa Victoria, hasa Mkoa wa Mara, maeneo ya mwambao wa pwani na maeneo ya nchi kavu, visiwa vya Unguja na Pemba pamoja na maeneo yenye miinuko katika Nyanda za Juu Kaskazini-Mashariki.

"Msimu wa Kipupwe wa mwaka 2026 unatarajiwa kutawaliwa na upepo wa Kusini Mashariki uliopungua nguvu kidogo kama ilivyo kawaida katika maeneo mengi ya nchi huku vipindi vya upepo mkali kutoka kusini vinatarajiwa kujitokeza zaidi katika miezi ya Juni na Julai, hasa katika maeneo ya ukanda wa pwani ya Bahari ya Hindi na maeneo ya nchi kavu. Amesema.

Amesema maeneo ya Kanda ya Ziwa Victoria yanatarajiwa kuwa na kiwango cha joto la chini kati ya nyuzi joto 10°C hadi 19°C, wakati Ukanda wa Pwani ya Kaskazini ikiwemo Dar es Salaam, Pwani, Tanga pamoja na Zanzibar unatarajiwa kuwa na kiwango cha nyuzi joto 18°C hadi 25°C kwa maeneo ya mwambao na visiwani.

Katika maeneo ya Nyanda za Juu Kusini-Magharibi, ambayo yanajumuisha Mbeya, Njombe, Songwe, Iringa na Rukwa, viwango vya joto la chini vinatarajiwa kufikia kati ya nyuzi joto 6°C hadi 21°C, huku maeneo ya miinuko yakitarajiwa kushuka chini ya nyuzi joto 5°C.

Dkt. Chang’a amesema, kufutia hali hiyo uwezekano wa kujitokeza kwa magonjwa yanayohusiana na hali ya baridi, ikiwemo homa ya mapafu kwa binadamu pamoja na magonjwa ya mifugo yanaweza kujitokeza vumbi litakalosababishwa na upepo katika baadhi ya maeneo linaweza kuongeza hatari ya magonjwa ya macho, mafua na matatizo mengine ya kiafya yanayohusiana na mfumo wa upumuaji.

Kwa wafugaji, mamlaka hiyo imeonya kuhusu uwezekano wa upungufu wa maji na malisho, huku ikiwataka kuendelea kufuata ratiba za kuogesha mifugo na ushauri wa wataalamu wa mifugo ma wakulima wameshauriwa kuzingatia ushauri wa maafisa ugani katika maeneo yatakayopata vipindi vya mvua nje ya msimu.

Sekta za ujenzi, uchukuzi na madini zinatarajiwa kunufaika na hali ya hewa ya msimu huo, huku watumiaji wa bahari wakitakiwa kufuatilia taarifa za hali ya hewa ili kupunguza athari za upepo unaotarajiwa.


Washiriki zaidi ya 300 wameshiriki mbio fupi za kilomita 5 katika  bonde la Olduvai Ngorongoro kwa lengo la kutangaza vivutio vya asili vya Olduvai na Laetoli ambapo historia ya Binadamu wa Kale ilianzia.

Akizungumza kwa Niaba ya Kamishna wa Uhifadhi kwenye tukio hilo, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi anayesimamia Huduma za Utalii na Masoko Mariam Kobelo ameeleza kuwa Ngorongoro kwa kushirikiana na Cape to Cairo Marathon imefanya mbio hizo ili kuonesha utajiri wa utalii wa asili, historia, urithi wa utamaduni na  mambo kale uliopo Olduvai na Laetoli kama Nyumbani kwa asili ya Binadamu. 

Ameongeza kuwa Ngorongoro ni Nyumbani kwa Nyumbu wanaohama kwa kuwa pumzi ya kwanza ya ndama kupigwa mhuri kabla ya kuhamia maeneo mengine safari yao huanzia Ndutu Ngorongoro.

"Ngorongoro ni Nyumbani kwa asili ya binadamu kisayansi, Ni nyumbani kwa Nyumbu wanaohama kila mwaka, ni nyumbani kwa Spinshi ya Ndege zaidi ya 500, ni nyumbani kwa Wanyama wakubwa watano, kiufupi eneo la Ngorongoro ni Nyumbani kwa mkusanyiko wa Vitu vingi ndio maana tunawaambia wadau wote ndani na nje ya Nchi kuwa Wonders Are Calling" ameongeza Kamishna Kobelo.

 Mkurugenzi wa Cape to Cairo Arusha International Marathon, Timothy Mdinka ameeleza kuwa lengo la mbio hizo ni kutangaza mazao mapya  ya Utalii yaliyopo Tanzania na Bara la Africa kwa Ujumla kupitia shughuli mbalimbali ikiwemo  Michezo kama mbio ambayo imefanyika leo Olduvai pamoja na marathon ya Cape to Cairo itakayofanyika tarehe 31 Mei, 2026.

Mbio hizo zimejumuisha wadau mbalimbali wakiwepo Ngorongoro, Cape to Cairo international Marathon, Karatu Runners,  Amani Collection, CRDB, UNDP, NHIF,  Diplomatic and Tourism Police Arusha.
















Na Janeth Raphael -MichuziTv Bungenin Dodoma

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Paschal Katambi Patrobass ameainisha vipaumbele nane (8) vitakavyotekelezwa na Wizara hiyo katika mwaka wa fedha 2026/27, vikilenga kuimarisha usalama wa raia, kuboresha utendaji wa vyombo vya usalama na kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma kwa wananchi.

Akizungumza wakati akiwasilisha hotuba ya makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara, Katambi amesema Serikali imejipanga kuendeleza mageuzi makubwa katika sekta ya usalama kwa kuzingatia mahitaji ya sasa ya kiutendaji na mabadiliko ya kiteknolojia.


Vipaumbele 8 vya Wizara 2026/27

Waziri Katambi ameeleza maeneo hayo ya kipaumbele kuwa ni:

1.Uboreshaji wa miundombinu ya vyombo vya usalama

Serikali itaendelea kuboresha miundombinu ya vyombo vya usalama chini ya Wizara, ikiwemo ujenzi na ukarabati wa makazi ya maafisa, wakaguzi, askari na watumishi wasio askari ili kuongeza ufanisi kazini.


2. Upatikanaji wa vitendea kazi

Kipaumbele kingine ni kuboresha upatikanaji wa vitendea kazi, hususan vyombo vya usafiri na usafirishaji kwa vyombo vya usalama ili kurahisisha utekelezaji wa majukumu ya kila siku.


3. Utafiti wa kiusalama

Wizara itaendelea kufanya tafiti mbalimbali kubaini sababu za makosa mapya ya jinai na kuweka mikakati madhubuti ya kuyakabili mapema.

4. Uimarishaji wa TEHAMA

Matumizi ya TEHAMA yataendelea kuimarishwa katika huduma zote zinazotolewa na Wizara na taasisi zake ili kuongeza ufanisi, uwazi na kasi ya huduma.

5. Mafunzo kwa watumishi na askari

Serikali itaendelea kuwajengea uwezo watumishi na askari kupitia mafunzo mbalimbali yanayolenga kuongeza weledi na ubora wa utekelezaji wa majukumu yao.

6. Miradi ya ujenzi wa NIDA

Wizara kupitia NIDA inatarajia kuanza ujenzi wa Makao Makuu yake jijini Dodoma, pamoja na ofisi 31 za usajili za wilaya na kituo cha mafunzo na matengenezo ya vifaa vya TEHAMA Kibaha.

7. Makazi ya waathirika wa usafirishaji haramu wa binadamu

Serikali pia itaanza ujenzi wa nyumba salama kwa ajili ya waathirika wa usafirishaji haramu wa binadamu jijini Dar es Salaam, ikiwa ni hatua ya kulinda haki na ustawi wa wahanga.

8. Uimarishaji wa shughuli za uzalishaji mali

Wizara itaendelea kuimarisha shughuli za uzalishaji mali kupitia kilimo, mifugo na viwanda, sambamba na kulinda na kuhifadhi mazingira.



Na Victor Masangu,Pwani 

Jumuiya ya umoja wa wanawake (UWT) Mkoa wa Pwani imeamua   kuwajengea uwezo na maharifa madiwani wote  wa viti maalumu kwa kuwapatia semina elezeki ambayo itawasaidia katika kutekeleza majukumu yao.

Katika semina hiyo ambayo pia imehudhuliwa na makatibu wa UWT ngazi za Wilaya imelenga kuwajengea uwezo ikiwa pamoja na kuwakumbusha wajibu na majukumu yao ya kila siku ya ndani ya chama na jumuiya.

Katibu wa  jumuiya ya wanawake (UWT) Mkoa wa Pwani Aziza Hussein amebainisha kwamba katika semina hiyo madiwani wamekumbushwa katika suala la kusimamia miradi ya maendeleo.

Pia katibu huyo amesema kwamba madiwani hao wameweza kupatiwa mbinu mbali ambazo zitaweza kuwasaidia katika kutatua changamoto ambazo zinawakabili wananchi.

"Tumeandaa semina hii ya kuwakutaniisha madiwani wote wa viti maalumu kutoka Mkoa wetu wa Pwani na lengo kubwa ni kuwajengea uwezo wa kutatua mambo mbali mbali ambayo wamekuwa wakiyatekeleza katika maeneo  yao,"amebainisha katibu huyo.

Kadhali amesema kwamba semina hiyo imewapa fursa ya kujifunza umuhmu wa  uwepo na bima ya afya kwa wote na namna bora ya kutambua kazi zao ikiwa pamoja na  kupendana na kuwa na umoja.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Jumuiya ya wanawake (UWT) Mkoa wa Pwani Zainabu Vullu amebainishs kwamba semina hiyo itakwenda kuwa msaada mkubwa kwa madiwani hao wa viti maalumu.

Mwenyekiti huyo amesema kwamba kwa sasa madiwani hao wanapaswa kuwa na umoja na mshikamano katika kuimarisha  uhai wa chama pamoja na jumuiya ya wanawake wa UWT Mkoa wa Pwani.

Nao baadhi ya madiwani wa viti maalumu akiwemo Tatu Mpeki kutoka Wilaya ya Mkuranga amesema semina hiyo waliyoipata itakuwa ni chachu kubwa na kwamba ameahidi kuyafanyia kazi yale yote ambayo wamefundishwa.

Pia ameupongeza uongozi wa UWT Mkoa wa Pwani kwa kuweza kuona umuhimu mkubwa wa kuwashirikisha madiwani wa viti maalumu ambao wameweza kupata elimu ambayo watakwenda  kuifanyia kazi kwa maslahi ya chama na jumuiya.

"Tunashukuru sana kwa dhati kwa uongozi wa UWT ngazi ya Mkoa kwa kuona umuhimu wa kutukutanisha kwa pamoja na kutupa semin hii ambayo kwetu ni hatua muhimu sana kwa sisi madiwani wa viti maalumu na kwamba tutayafanyia kazi yale yote ambayo tumefundishwa,"amesema Mhe.Tatu.

Semina ya madiwani wa viti maalumu Mkoa wa Pwani imeandaliwa na  uongozi wa Jumuiya wa wanawake (UWT) Mkoa wa Pwani kwa lengo la kuwajengea uwezo na kuwapa mbinu mbali mbali ambazo zitawasaidia katika utekelezaji  wa majukumu yao ya chama na jumuiya.






Na Janeth Raphael MichuziTv Bungeni - Dodoma

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Paschal Katambi Patrobass amesema Serikali imeendelea kuimarisha ulinzi na usalama wa raia pamoja na mali zao kupitia operesheni mbalimbali zinazofanywa na Jeshi la Polisi kwa kushirikiana na vyombo vingine vya ulinzi na usalama nchini.

Katambi ameyasema hayo leo bungeni jijini Dodoma wakati akiwasilisha hotuba ya makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa mwaka wa fedha 2026/2027.

Amesema katika kipindi cha Julai 2025 hadi Aprili 2026, Wizara kupitia Jeshi la Polisi imeendelea kufanya doria, misako na operesheni maalum zenye lengo la kubaini, kuzuia na kutanzua vitendo vya uhalifu katika maeneo mbalimbali nchini.

Kwa mujibu wa Waziri huyo, ushirikiano kati ya Jeshi la Polisi, vyombo vya ulinzi na usalama pamoja na wananchi umechangia kwa kiasi kikubwa kuendelea kuwepo kwa hali ya amani na utulivu nchini, jambo ambalo limewawezesha wananchi kuendelea na shughuli zao za kiuchumi na kijamii kwa utulivu.

Aidha, Katambi amesema Serikali inaendelea kutoa elimu kwa umma kuhusu utekelezaji wa falsafa ya Polisi Jamii ili kuongeza ushiriki wa wananchi katika mapambano dhidi ya uhalifu.

Katika takwimu alizowasilisha bungeni, Katambi amesema makosa makubwa ya jinai yaliyotolewa taarifa katika vituo vya Polisi nchini yamepungua katika kipindi hicho.

Amesema kuanzia Julai 2025 hadi Aprili 2026 jumla ya makosa makubwa ya jinai 39,027 yaliripotiwa katika vituo vya Polisi, ikilinganishwa na makosa 40,022 yaliyorekodiwa katika kipindi kama hicho mwaka 2024/2025.

Katambi alieleza kuwa kupungua kwa makosa hayo kunatokana na kuongezeka kwa uelewa wa wananchi pamoja na ushirikiano wa jamii katika kubaini na kuzuia vitendo vya uhalifu kabla havijatokea au kusababisha madhara makubwa.

Akifafanua zaidi kuhusu aina za makosa yaliyorekodiwa, Waziri huyo alisema makosa 9,603 yalikuwa dhidi ya binadamu, makosa 13,986 yalihusiana na maadili ya jamii, makosa 14,794 yalikuwa ya kuwania mali huku makosa 644 yakihusiana na uhalifu wa kifedha.

Waziri Katambi alisisitiza kuwa Serikali itaendelea kuimarisha mifumo ya usalama, kuongeza uwezo wa vyombo vya dola pamoja na kuendeleza ushirikiano na wananchi ili kuhakikisha Tanzania inaendelea kuwa salama na yenye utulivu wakati wote.




Kumekuwa na mwitikio mkubwa wa watalii wa ndani kutembelea hifadhi ya Ngorongoro hii ikimaanisha wanarudi nyumbani eneo ambalo ndilo pekee lenye ushahidi wa kisayansi usiotiliwa shaka kuwa ndio chanzo cha binadamu wa kale.

Safari hii ni zamu ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT ) chini ya Mchungaji Kiongozi wa Kanisa  hilo Usharika wa Kijitonyama jijini Dar es Salaam Rev, Dr. Elliona Kimaro aliyeongoza kundi la wanaume 300 kutoka mikoa mbalimbali nchini kutembea Makumbusho ya Jiopaki ya Ngorongoro-Lengai (Urithi Geopark) na vituo vya hifadhi vilivyopo Ngorongoro 

Akiwa na Ujumbe huo Dkt.  Kimaro amesema makundi mbalimbali kuhamasika kufanya utalii wa Ndani wanavutiwa na vitu mbalimbali ikiwemo kushuhudia uumbaji wa Mungu, kuona na kujifunza Chanzo cha asili ya Mwanadamu katika bonde la Olduvai na Laetoli, kuona Ikolojia ya hifadhi pamoja na utunzaji wa Mazingira kama vitabu vitakatifu vinavyohimiza.

"Tumekuja Nyumbani Ngorongoro kwenye asili ya Mwanadamu tukiwa na kundi la wanaume 300,  tumeshuhudia uumbaji wa Mungu, utunzaji wa Ikolojia, Mazingira, Misitu Wanyama wa kila aina ya vyote vilivyoumbwa kwa mfano wa Mungu" alisema  Dkt. Kimaro.

Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro inawarudisha nyumbani binadamu wote ili kushuhudia asili yao ambapo binadamu alianza kutembea na kufanya shughuli zake kwa miguu miwili.







Na Janeth Raphael MichuziTv Bungeni - Dodoma

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Paschal Katambi Patrobass ameliomba Bunge kuidhinisha jumla ya Shilingi trilioni 2.44 kwa ajili ya matumizi ya Wizara hiyo katika mwaka wa fedha 2026/2027.

Akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara hiyo Kwa mwaka  2036/2027 bungeni leo, Waziri Katambi amesema wizara inaomba kuidhinishiwa jumla ya Shilingi 2,443,215,927,000 kwa ajili ya utekelezaji wa majukumu mbalimbali ya kiusalama, kiutawala na maendeleo nchini.

Katambi ameeleza kuwa kati ya fedha hizo, Shilingi 1,953,366,486,000 sawa na asilimia 80 ya bajeti yote ya wizara zitatumika kwa Matumizi ya Kawaida.

Amefafanua kuwa ndani ya fedha hizo, Shilingi 1,183,766,640,000 zimetengwa kwa ajili ya mishahara ya watumishi, huku Shilingi 769,599,846,000 zikielekezwa kwenye matumizi mengineyo ya wizara na taasisi zake.

Aidha, Waziri huyo amesema Shilingi 489,849,441,000 sawa na asilimia 20 ya bajeti yote zimetengwa kwa ajili ya Miradi ya Maendeleo.

Kwa mujibu wa Katambi, kati ya fedha za maendeleo, Shilingi 453,955,843,000 ni fedha za ndani huku Shilingi 35,893,598,000 zikiwa ni fedha za nje zitakazosaidia utekelezaji wa miradi mbalimbali chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.

Waziri Katambi amesisitiza kuwa fedha hizo zitawezesha wizara kuendelea kuimarisha usalama wa raia na mali zao, kuboresha miundombinu ya vyombo vya ulinzi na usalama pamoja na kuongeza ufanisi wa utoaji huduma kwa wananchi.

Hotuba hiyo imewasilishwa bungeni leo wakati wa mjadala wa makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa mwaka wa fedha 2026/2027.



 

 

Katika kuelekea kilele cha maadhimisho ya Jubilei ya Dhahabu ya miaka 50 ya Maonesho ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), mwaka huu wadau wa biashara, wawekezaji, wabunifu na wananchi wanatarajiwa kushuhudia tukio la kipekee la kihistoria litakalojulikana kama “Sabasaba Golden Night”, Usiku wa Tuzo utakaofanyika tarehe 6 Julai 2026, usiku huu maalum wa dhahabu unalenga kusherehekea mafanikio, ubunifu na mchango wa maonesho hayo katika kukuza biashara na uchumi wa Tanzania kwa zaidi ya nusu karne.

Aidha,Uzinduzi wa Sabasaba Golden Night umebeba taswira mpya ya Maonesho ya Sabasaba ya mwaka 2026, ukiahidi burudani ya kiwango cha juu, mwangaza wa kipekee, maonesho ya kisasa, kutambua wadau waliotoa mchango mkubwa katika safari ya miaka 50 pamoja na kuunganisha sekta za biashara, uwekezaji na ubunifu chini ya jukwaa moja. Tukio hilo linatarajiwa kuwa moja ya vivutio vikubwa ndani ya Maonesho ya 50 ya Jubilei ya Dhahabu, yakiyotarajiwa kufanyika kuanzia tarehe 28 Juni hadi 13 Julai, 2026.

Akizungumza Mgeni Rasmi Mhe. Dennis Londo amesema Tuzo hizo zitakazotolewa Mwaka huu zinalenga kuonesha ni kwa namna gani Sekta ya Biashara imekua kupitia maonesho ya Biashara ya Sabasaba na namna ambavyo Maonesho haya yamekuza maelfu ya wafanyabiashara amba sasa ni wakubwa.

Aidha Dkt.Latifa Mohammed Khamis Mkurugenzi Mkuu wa Maendeleo ya Biashara Tanzania ameeleza kuwa “Usiku wa Dhahabu” si burudani pekee, bali ni ishara ya heshima kwa safari ya mafanikio ya Sabasaba tangu kuanzishwa kwake, sambamba na kufungua ukurasa mpya wa fursa za biashara, teknolojia na ushirikiano wa kimataifa. Wageni watakaohudhuria watapata nafasi ya kushuhudia historia ikikutana na ubunifu wa kizazi cha sasa katika mazingira yatakayobeba hadhi ya Jubilei ya Dhahabu. “Sabasaba 2026 KUBWA KULIKO

Na; Mwandishi Wetu, Unguja

WAZIRI  wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni amesema msimu ujao wa Ligi ya Muungano utaboreshwa zaidi ikiwa pamoja na zawadi kwa bingwa ili kuipa hadhi ya kipekee ligi hiyo.

Amesema lengo ni kuifanya ligi hiyo inakuwa moja ya ligi bora Afrika Mashariki na kuifanya kuwa na mvuto wa aina yake kwa wapenda soka akieleza kuwa michezo ndio sehemu ambayo jamii hukutana na kuongea lugha moja.

Mhe. Masauni ameyasema hayo Mei, 24, 2026 Unguja, Zanzibar wakati wa halfa ya utoaji tuzo na zawadi kwa walioshiriki na kufanikisha Ligi ya Muungano 2026 ambapo Simba ilitawazwa mabingwa kwa kuifunga Yanga bao 1-0 katika mchezo uliochezwa Uwanja wa Amaan Complex.

“Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar zimeendelea kuchukua hatua madhubuti za kuimarisha Muungano kwa misingi ya Kikatiba, Kihistoria, Mshikamano wa Kitaifa na maendeleo ya pamoja.

“Juhudi hizo zinajielekeza kuhakikisha kuwa jamii ya Watanzania inakuwa na umoja na ushirikiano katika nyanja zote za kiuchumi, kijamii na kisiasa.

Mhe. Masauni amesema, Ofisi ya Makamu wa Rais ambayo ndiyo yenye dhamana na masuala ya Muungano kwa kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeamua kuwa sehemu ya uratibu wa Ligi ya Muungano ili kuongeza nguvu.

Amesema hatua hii itasaidia kuboresha maandalizi ya ligi ikiwemo kuboresha zawadi kwa washiriki na mshindi wa ligi.

“Nizipongeze timu zote ambazo zilishiriki mashindano haya kwa mwaka 2026 maana ushiriki wao ndio mafanikio ya uwepo wa Ligi hii ya Muungano.”

Kwa upande wake, Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo Zanzibar, Dkt. Riziki Pembe Juma amesema pamoja na ligi hiyo kusimama kwa muda mrefu lakini ilipotangazwa kurejea wadau waliitikia vizuri na kutoa ushirikiano.

“Awali kama wizara tulianza kwa wasiwasi lakini mwisho tulimaliza kwa furaha kwani tumegundua michezo imekuwa kitu cha kipekee na tutazidi kushirikiana na kumalizika kwa msimu huu inafanya tuanze maandalizi kwa ajili ya mwaka ujao,” amesema Mhe. Dkt. Riziki.

Naye, Katibu Mkuu wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Zanzibar (ZFF), Hussein Ahmada amezishukuru serikali za pande zote mbili kwa kuifanya michezo kuwa moja ya eneo la kuwaunganisha Watanzania kupitia Ligi ya Muungano akieleza kuwa hali hiyo imekuwa faraja kwa wapenda soka kuona nao wanathaminiwa.

Mwaka huu ligi hiyo ilishirikisha timu nane ambazo ni Simba iliyotwaa ubingwa, Yanga, Azam na Singida Black Stars kutoka Tanzania Bara wakati kwa Zanzibar ilikuwa Mlandege, KVZ, Mafunzo na Muembe Makumbi.


Na Janeth Raphael MichuziTv Bungeni- Dodoma.

Serikali imesema kuwa Makao yote ya Watoto nchini yanaanzishwa na kuendeshwa kwa kuzingatia sheria, kanuni na miongozo maalum inayolenga kuhakikisha watoto wanaolelewa katika vituo hivyo wanaishi katika mazingira salama, yenye ulinzi na malezi bora.

Kauli hiyo imetolewa leo Mei 25, 2026 bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Maryprisca Winfried Mahundi wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Lucy Simirya Kombani ambaye alitaka kujua ni utaratibu gani unaotumiwa na Serikali kuhakikisha watoto wanaoishi katika vituo vya kulelea watoto wanapata mazingira bora na salama.

Akijibu swali hilo, Mahundi amesema Makao yote ya Watoto yanaanzishwa kwa mujibu wa Sheria ya Mtoto Sura ya 13, Kanuni za Makao ya Watoto za mwaka 2012 pamoja na Mwongozo wa Taifa wa Uanzishaji, Uendeshaji na Usimamizi wa Makao ya Watoto wa mwaka 2024.

Amesema utaratibu wa kuanzisha Makao ya Watoto huanzia ngazi ya Kata ambapo maombi hupokelewa na kufanyiwa tathmini kabla ya kuwasilishwa katika ngazi ya Halmashauri na hatimaye kupelekwa Wizarani kwa Kamishna wa Ustawi wa Jamii kwa ajili ya kupata leseni ya usajili.

“Makao hayo hupatiwa usajili rasmi pale yanapokidhi vigezo na masharti yote yaliyowekwa na Serikali kwa ajili ya kuhakikisha watoto wanapata huduma stahiki za malezi, ulinzi na maendeleo yao kwa ujumla,” amesema Mahundi.

Aidha, Naibu Waziri huyo ameeleza kuwa Serikali imeendelea kuimarisha usimamizi wa Makao ya Watoto kupitia Maafisa Ustawi wa Jamii waliopo katika ngazi mbalimbali kuanzia Wizara, Mkoa hadi Halmashauri.

Kwa mujibu wa Mahundi, Maafisa hao hufanya ukaguzi na ufuatiliaji wa mara kwa mara katika vituo vya kulelea watoto ili kuhakikisha huduma zinazotolewa zinazingatia viwango vya ubora pamoja na kulinda haki na usalama wa watoto wanaolelewa humo.

Amesisitiza kuwa Serikali haitaruhusu uwepo wa Makao ya Watoto yanayokiuka taratibu, sheria na miongozo iliyowekwa kwani lengo kuu ni kuhakikisha watoto wote wanaopata huduma katika vituo hivyo wanalelewa katika mazingira yenye upendo, usalama na ustawi unaostahili.

Kauli hiyo imekuja wakati Serikali ikiendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuimarisha mifumo ya malezi na ulinzi wa watoto nchini, sambamba na kuhakikisha taasisi zote zinazohusika na huduma za watoto zinafanya kazi kwa kuzingatia sheria na misingi ya haki za mtoto.




Na Ashura Mohamed, Karatu


Bodi ya Wakurugenzi wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) imeridhishwa na hatua iliyofikiwa katika utekelezaji wa Mradi wa Utafiti wa Mafuta na Gesi wa Eyasi-Wembere uliopo Wilaya ya Karatu, Mkoa wa Arusha.

Ziara hiyo ya ukaguzi iliongozwa na Mwenyekiti wa Bodi ya TPDC, Balozi Ombeni Sefue, ambaye alisema shirika limepiga hatua kubwa kwa kuhakikisha kazi nyingi za kitaalamu sasa zinafanywa na wataalamu na wakandarasi wazawa wa Kitanzania.

Kwa mujibu wa Balozi Sefue, awali baadhi ya kazi hizo zilikuwa zikifanywa na makampuni ya nje ya nchi, lakini sasa TPDC imeweka mkazo kwa wazawa ili kujenga uwezo wa kitaalamu ndani ya nchi.

“Kazi nyingi za kitaalamu sasa zinafanywa na vijana waliopo hapa nchini kwa ubora unaotakiwa ikiwa ni pamoja na wakandarasi wazawa ambao wameajiriwa na TPDC,” alisema Balozi Sefue.

Akizungumzia matumizi ya fedha katika mradi huo, Balozi Sefue alibainisha kuwa hadi sasa zaidi ya shilingi bilioni 47 zimetumika tangu mradi uanze mwaka 2015 hadi mwaka 2026. Alifafanua kuwa fedha hizo zimetoka ndani ya TPDC, kutokana na imani kuwa utafiti huo utatoa matokeo chanya yatakayonufaisha taifa.

“Sasa utafutaji wa mafuta una hatua nyingi kwa sababu ni gharama kubwa sana kuchimba visima vya mafuta. Huwezi kuanza kuchimba kabla ya kufanya hatua ya kwanza ikakupa matumaini, halafu unaenda hatua ya pili na ya tatu mpaka mwisho unachimba kisima cha majaribio ili kupata matokeo chanya,” alieleza.

Balozi Sefue alitaja changamoto zinazokabili mradi huo kuwa ni pamoja na eneo la Ziwa Eyasi kuwa na tope na wakati mwingine ziwa kuka, hali inayochelewesha utekelezaji wa kazi licha ya mkandarasi kuwa na vifaa vya kisasa.

Kwa upande wake, Meneja wa Mradi wa Eyasi-Wembere, kutoka TPDC,Sindi Maduhu, alisema sasa mradi upo katika hatua ya kuchukua data za mitetemo na wanatarajia kukamilisha awamu ya kwanza ifikapo mwezi Juni 2026.

Aliongeza kuwa kazi hiyo inatekelezwa na mkandarasi mzawa, Kampuni ya African Geophysical Service (AGS), ambayo imepata mafanikio makubwa kutokana na matumizi ya wataalamu wenye ujuzi na mitambo ya kisasa inayolingana na mazingira ya eneo hilo.

Mradi wa Eyasi-Wembere unapitiwa pia na bomba la mafuta la Afrika Mashariki (EACOP), jambo linalotarajiwa kuwezesha usafirishaji wa mafuta yatakayopatikana na kuongeza kasi ya shughuli za utafiti katika eneo hilo.
Meneja wa mradi kutoka TPDC Sindi Maduhu akitoa maelekezo kwa Kamati ya Bodi ya Wakurugenzi TPDC


Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi TPDC Balozi Ombeni Sefue akiwa katika Ziwa Eyasi wakati wa Ukaguzi wa MRADI WA Eyasi-Wembere



Na Mwandishi Wetu
SHULE ya St Anne Marie Academy iliyoko Mbezi Kimara kwa Msuguri jijini Dar es Salaam mwaka huu inatimiza miaka 25 yenye mafanikio makubwa kwenye utoaji wa elimu bora tangu kuanzishwa kwake.

Tarehe 18 Julai mwaka huu itatimiza miaka 25 ikiwa ni miongoni mwa shule bora nchini ambazo zimekuwa zikifanya vizuri kwenye matokeo ya kitaaluma kuanzia ngazi ya kata, Wilaya, Mkoa hadi kwenye ngazi ya taifa.

Hayo yalisemwa mwishoni mwa wiki na Mbunge wa Bukoba Vijijini (CCM), ambaye pia ni Mkurugenzi Mwanzilishi wa shule hizo Dkt. Jasson Rweikiza wakati akizungumza kuhusu miaka 25 ya kutoa huduma ya elimu.

Dkt Rweikiza alisema miongoni mwa mafanikio makubwa ya shule hiyo kwa miaka 25 ni kutoa mwanafunzi bora kitaifa katika matokeo ya darasa la saba yaliyotangazwa na Baraza la Taifa la Mitihani NECTA mwaka 2021.

Alisema licha ya kutoa mwanafunzi bora kitaifa mwaka 2021, shule hiyo imekuwa ikifanikiwa kuingiza wanafunzi wengi kwenye 10 bora kitaifa kwa miaka mingi na imepata pongezi nyingi kitaifa na kimataifa.

“Upekee wa shule yetu ya St Anne Marie Academy ni kuwa na miundombinu bora kama maktaba zenye viyoyozi zilizosheheni vitabu vya kila aina, maabara za kisasa za sayansi zinazowawezesha wanafunzi wa masomo ya sayansi kusoma kwa vitendo,” alisema Dk Rweikiza.

Aidha, alisema St Anne Marie Academy ni shule ya kwanza na ya pekee nchini kuanzisha utaratibu wa kuwasomesha bure hadi kumaliza masomo yao wanafunzi wa shule hiyo wanaofiwa na mzazi anayelipa ada.

“Tumekuwa tukiahidi na kutekeleza kwamba hakuna mwanafunzi atakayefukuzwa shule kwa kukosa ada baada ya kufiwa na mzazi aliyekuwa akilipa ada, kama mwanafunzi yuko darasa la kwanza basi atasoma hadi darasa la saba na kama yuko kidato cha kwanza basi atamaliza kidato cha nne,” ni kauli ya Dk Rweikiza ambayo amekuwa akiitoa mara kwa mara kwenye mahafali shuleni hapo.

Dkt Rweikiza alisema matokeo bora ya shule hiyo ni jambo ambalo halijatokea kwa bahati bali ni kutokana na moundombinu bora iliyowekwa ikiwemo bodi ya mitihani ndani ya shule hiyo.

“Ili kuongeza ufanisi wa kitaaluma, kazi ya kutunga mitihani shuleni kwetu St Anne Marie Academy imekuwa ikifanywa na bodi hiyo ya mitihani na walimu wanakuwa na kazi ya kufundisha tu hali ambayo imeongeza ufaulu kwa kiwango kikubwa,” alisema

“Walimu wa St Anne Marie Academy tumewaachia kazi ya kufundisha tu, kazi ya kutunga mitihani ni ya bodi ya mitihani na tangu tuanzishe utaratibu huu tumeona mafanikio makubwa sana ya kuongezeka kwa ufaulu wa wanafunzi wetu,” alisema Dk Rweikiza

 

Meneja wa Bidhaa wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. George Kaindoah, akimkabidhi tuzo Malachi Mwiki, mmoja wa washindi wa mashindano ya kuogelea ya Swahili Talent Swimming, yaliyodhaminiwa na Benki ya Absa na kumalizika jana katika viwanja vya Gymkhana Club jijini Dar es Salaam. Mashindano hayo yalishirikisha zaidi ya washiriki 300 kutoka shule zaidi ya 25, huku yakitoa kipaumbele maalum katika kuhamasisha ushirikishwaji kwa kuwajumuisha watoto wenye mahitaji maalum kutoka Dar es Salaam na Arusha, kwa lengo la kutambua na kukuza vipaji vya vijana katika mchezo wa kuogelea.
Muogeleaji chipukizi Cairo Erick Johannes, akionesha umahiri wake wakati wa mashindano ya kuogelea ya Swahili Talent Swimming, yaliyodhaminiwa na Benki ya Absa Tanzania na kumalizika jana katika viwanja vya Gymkhana Club jijini Dar es Salaam. Mashindano hayo yalishirikisha zaidi ya washiriki 300 kutoka shule zaidi ya 25, huku yakilenga kuhamasisha ushirikishwaji kwa kuwajumuisha watoto wenye mahitaji maalum kutoka Dar es Salaam na Arusha, kwa lengo la kutambua na kukuza vipaji vya vijana katika mchezo wa kuogelea.
Meneja wa Bidhaa wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. George Kaindoah, akimkabidhi tuzo Amran Suleiman, mmoja wa washindi wa mashindano ya kuogelea ya Swahili Talent Swimming, yaliyodhaminiwa na Benki ya Absa na kumalizika jana katika viwanja vya Gymkhana Club jijini Dar es Salaam. Washindi wengine wanaoonekana pichani ni Alssein Humudi (wa tatu kushoto) na Konhelli Mhella. Mashindano hayo yalishirikisha zaidi ya washiriki 300 kutoka shule zaidi ya 25, huku yakilenga kuhamasisha ushirikishwaji kwa kuwajumuisha watoto wenye mahitaji maalum kutoka Dar es Salaam na Arusha, kwa lengo la kutambua na kukuza vipaji vya vijana katika mchezo wa kuogelea.
Waogeleaji wakichuana wakati wa mashindano ya kuogelea ya Swahili Talent Swimming yaliyodhaminiwa na Benki ya Absa Tanzania na kumalizika jana katika viwanja vya Gymkhana Club jijini Dar es Salaam. Mashindano hayo yalishirikisha zaidi ya washiriki 300 kutoka shule zaidi ya 25, huku yakilenga kuhamasisha ushirikishwaji kwa kuwajumuisha watoto wenye mahitaji maalum kutoka Dar es Salaam na Arusha, kwa lengo la kutambua na kukuza vipaji vya vijana katika mchezo wa kuogelea.
Baadhi ya washiriki wenye mahitaji maalumu, wakipozi kwa picha ya kumbukumbu na Irene Mushi kutoka Benki ya Absa, baada ya kuwakabidhi medali zao, wakati wa mashindano ya kuogelea ya Swahili Talent Swimming, yaliyodhaminiwa na Benki ya Absa na kumalizika jana katika viwanja vya Gymkhana Club jijini Dar es Salaam. Mashindano hayo yalishirikisha zaidi ya washiriki 300 kutoka shule zaidi ya 25, huku yakilenga kuhamasisha ushirikishwaji kwa kuwajumuisha watoto wenye mahitaji maalum kutoka Dar es Salaam na Arusha, kwa lengo la kutambua na kukuza vipaji vya vijana katika mchezo wa kuogelea.

Muogeleaji chipukizi Malikah Kassim akionesha medali yake wakati wa mashindano ya kuogelea ya Swahili Talent Swimming  yaliyodhaminiwa na Benki ya Absa Tanzania na kumalizika jana  katika viwanja vya Gymkhana Club, jijini Dar es Salaam.  Mashindano hayo yalishirikisha zaidi ya washiriki 300 kutoka shule zaidi ya 25, huku yakilenga kuhamasisha ushirikishwaji kwa kuwajumuisha watoto wenye mahitaji maalum kutoka Dar es Salaam na Arusha, kwa lengo la kutambua na kukuza vipaji vya vijana katika mchezo wa kuogelea.

Baadhi ya washindi wa mashindano ya kuogelea ya Swahili Talent Swimming Competition Season 3 yaliyomalizika jana, wakionesha medali zao wakati wa hafla ya utoaji wa tuzo katika viwanja vya Gymkhana Club, jijini Dar es Salaam. Mashindano hayo yalishirikisha zaidi ya washiriki 300 kutoka shule zaidi ya 25, huku yakilenga kuhamasisha ushirikishwaji kwa kuwajumuisha watoto wenye mahitaji maalum kutoka Dar es Salaam na Arusha, kwa lengo la kutambua na kukuza vipaji vya vijana katika mchezo wa kuogelea.

 


Top News