NA EMMANUEL MBATILO, BAGAMOYO

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Adolf Mkenda, amewataka Wathibiti Ubora wa Shule kuhakikisha wanatoa taarifa kwa wakati kuhusu changamoto zinazoikabili sekta ya elimu, ikiwemo ukosefu wa vifaa na madarasa, ili hatua stahiki zichukuliwe haraka.

Akizungumza leo Februari 17, 2026 wilayani Bagamoyo, mkoani Pwani, wakati wa ufunguzi wa mafunzo elekezi ya Wathibiti Ubora wa Shule ngazi ya wilaya, Prof. Mkenda amesema jukumu la wadhibiti hao ni muhimu katika kubaini na kuwasilisha mapungufu yanayojitokeza shuleni.

Amesema Wathibiti Ubora wanapaswa kuwasilisha taarifa hizo kwa Wakurugenzi na Wakuu wa Wilaya ili kuwezesha mamlaka husika kuchukua hatua za haraka za utatuzi.

Aidha, Waziri Mkenda amesisitiza kuwa dhamira kuu ya Wathibiti Ubora wa Shule ni kuhakikisha utekelezaji wa sera, sheria, miongozo na mikakati ya elimu unafanyika kwa ufanisi na kwa kuzingatia viwango vilivyowekwa.

Amewataka watendaji hao kusaidia kikamilifu utekelezaji wa sera za elimu na kuhakikisha wanazielewa kwa undani, hususan sera zinazohusu elimu ya amali na elimu ya lazima.

Akizungumzia mageuzi ya Sekta ya Elimu, Prof. Mkenda amesema kuwa kuanzia mwaka wa masomo 2027/2028, elimu ya msingi itatolewa kwa miaka sita badala ya saba, huku elimu ya lazima ikiongezwa kuwa miaka kumi, kuanzia darasa la kwanza hadi kidato cha nne.

“Mabadiliko haya yataleta ‘double cohort,’ ambapo wanafunzi wa darasa la saba (mfumo wa zamani) na darasa la sita (mfumo mpya) wataingia kidato cha kwanza kwa wakati mmoja. Hata hivyo, hali hiyo ni ya mpito na mfumo utarejea katika ‘single cohort’ baada ya muda,” amefafanua.

Waziri Mkenda ameongeza kuwa Serikali inaendelea kuwekeza katika shule za ufundi, lakini bado kuna changamoto ya uhaba wa karakana, vifaa na walimu wenye sifa.

Amezitaka Halmashauri kupanga bajeti kwa umakini ili kuhakikisha shule hazifungwi kutokana na ukosefu wa mahitaji ya msingi.








Balozi Wilson Masilingi amesema kuwa masuala ya Uwazi na Uwajibikaji ni muhimu sana kwa manufaa ya wananchi,kwa kizazi cha sasa na hata kizazi kijacho.

Balozi Masilingi ameyasema hayo Jijini Dodoma Februari 17,2026 mara baada ya kupokewa katika Taasisi ya Uhamasishaji Uwazi na Uwajibikaji katika Rasilimali Madini,Mafuta na Gesi Asilia (TEITI) ambapo amepokewa kuwa Mwenyekiti wa Bodi hiyo.

Na kuongeza kuwa moja ya majukumu ya Taasisi hiyo ni pamoja na kuelimisha na kuwataarifu wananchi kuhusu mambo wanayoyafanya na matokeo yake na manufaa yaliyopo kwao.

"Kwasababu moja ya majukumu yetu ni kuwataarifu na kuelimisha wananchi waliotupatia jukumu hili kuhusu mambo ambayo tunafanya na matokeo yake na yana manufaa gani kwao na wanaweza kuchangia nini kuyaboresha kwa manufaa yao kwa kizazi cha sasa na kijacho,kama mnavyofahamu masuala ya Uwazi na Uwajibikaji ni muhimu sana sana".

Aidha ameahidi katika Uongozi wake kupitia Mtendaji Mkuu wa Taasisi hiyo kuanza na Vijana walioko mtaani wenye taaluma kwenye masuala ya Madini,Mafuta na Gesi asilia kujisajili katika Website yao na wao kuona namna ya kuweza kuwafikia na kutafuta namna ya kuwafundisha zaidi ili waweze kusaidia kupata taarifa na kuhamasisha Umma ili kuondokana na jamii isiyoelewa mambo hayo.

Pamoja na hayo amesema anaamini Watumishi wa Taasisi hiyo watampatia ushirikiano kama walivyowapa watangulizi wake katika kutekeleza majukumu ambayo wamepewa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa niaba ya wananchi wake.

Pia Balozi Masilingi amewataka Watumisha hao kufanya kazi kwa bidii,umoja, kushirikiana na upendo kwani kwa kufanya hivyo kutaepusha kuwepo kwa migongano.

Mhe Balozi Wilson Masilingi ni Mwenyekiti wa 3 tangu kuanzishwa kwa Bodi hiyo ya TEITI.









Chama Cha Mapinduzi kimesema kukamilika kwa mradi wa maji  ya Ziwa Victoria unakwenda kuwa mkombozi kwa wananchi wa Urambo, Sikonge na Kaliua.

Katibu wa NEC Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa CCM Taifa Kenani Kihongosi amesema hayo wakati alipokagua maendeleo ya ujenzi wa mradi huo unaogharimu kiasi cha  Sh bilioni 143.

"Niseme kwa dhati Urambo ilikuwa na changamoto kubwa ya maji, maji yalikuwa ni shida lakini serikali ya CCM iliahidi kwenye ilani yake kwamba itakwenda kujenga mtandao mkubwa wa maji ambao ni gridi ya maji ya taifa kama ambavyo tulivyo na gridi ya umeme kwa hiyo kila kijiji kitapata maji safi na salama,"alisema.

Kadhalika Kihongosi alimtaka Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Maji safi na Usafi wa Mazingira Tabora (TUWASA) Mayunga Kashirimu kukamilisha kazi iliyobaki ndani ya siku 14 ili wananchi waanze kupata huduma ya maji safi na salama.

Ujenzi wa mradi huo unahusisha kulaza mabomba kwa urefu wa kilometa 190, kujenga matangi matano yakiwemo makubwa matatu yenye uwezo wa kubeba lita milioni mbili na kufunga viungio vya mabomba ambapo mpaka sasa wamebakiza mita 220 kukamilisha kazi iliyobaki.









Na Janeth Raphael MichuziTv Kondoa - Dodoma

Naibu Waziri wa Nishati Salome Makamba amewataka Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kuchochea matumizi ya Nishati safi ya kupikia katika maeneo ya minada, stendi na masoko. kwani tafiti zinaonesha kuwa kuna minada ya awali na upili ipatayo 13,763 pamoja na masoko ya samaki yapatayo 1,229 nchini, ambayo yanapaswa kufikiwa kutokana na kuhudumia kundi kubwa la wananchi.

Naibu Waziri huyo ameyazungumza hayo leo Kondoa, Dodoma wakati akizindua awamu ya kwanza ya mradi wa kusambaza nishati safi ya kupikia katika taasisi zinazohudumia watu zaidi ya 100, unaohusisha shule 52 za sekondari pamoja na chuo kimoja cha Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) katika mikoa 18 ya Tanzania Bara.

Amesisitiza uwekaji wa miundombinu ya nishati safi ya kupikia katika shule zote za umma na binafsi ili kutimiza azma ya Serikali kwa taasisi zinazohudumia zaidi ya watu 100 kutumia nishati hiyo.

Ameeleza kuwa katika awamu ya kwanza, taasisi 53 zitanufaika, huku awamu ya pili ikihusisha taasisi 400 zilizopo katika mikoa yote nchini.

Ametanabaisha kuwa, kuwepo kwa mradi huo ni utekelezaji wa azma ya Serikali inayoongozwa na Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha taasisi zote zinazohudumia watu zaidi ya 100 zinatumia nishati safi ya kupikia.

"Ili mradi huu uwe endelevu, nitoe wito kwa Serikali za Mitaa, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia pamoja na TAMISEMI kusimamia mifumo iliyofungwa ili iwe endelevu suala litakalohamasisha jamii kuiga mfano wa taasisi za umma kuhamia katika nishati safi ya kupikia.” amesema Mhe. Salome

Aidha, ameitaka sekta binafsi kuona na kuchangamkia fursa iliyopo katika uzalishaji na usambazaji wa nishati safi ya kupikia ili kuongeza upatikanaji na kupunguza gharama kwa wananchi.

Kwa walimu na wanafunzi, ametoa wito wawe mabalozi wa mabadiliko kwa kuanzisha klabu za nishati safi ya kupikia shuleni ili kupeleka ujumbe huo katika familia na jamii zinazowazunguka.

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Mhe. Jonas Mbunda, amemshukuru Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuanzisha na kugharamia mpango wa nishati safi ya kupikia, akieleza kuwa unalinda afya za wananchi na mazingira.

Naye, Mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati ambaye ni Mkurugenzi wa Nishati Safi ya Kupikia, Nolasco Mlay, amesema mradi huo utapunguza matumizi ya kuni na mkaa katika taasisi za elimu, kuchangia uhifadhi wa mazingira, kuboresha afya na usalama wa wapishi pamoja na kuongeza ufanisi wa uendeshaji wa shule.

Aidha, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa REA, Mhandisi Jones Olotu, amesema takwimu zinaonesha kuwa matumizi ya nishati isiyo safi yamepelekea takribani hekta 46,606 za misitu kuharibiwa kila mwaka kwa ajili ya kuni na mkaa, watu zaidi ya 33,000 wakifariki kutokana na matumizi ya nishati isiyo safi ya kupikia na wanawake na watoto wa kike kutumia saa 4 hadi 8 kutafuta kuni, jambo linaloathiri muda wa shughuli za maendeleo.

Amesema Serikali ilitambua changamoto hizo na hivyo kuja na mkakati wa nishati safi ya kupikia ili kulinda mazingira, afya na muda wa kufanya shughuli za maendeleo.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Nishati Jadidifu na Teknolojia za Nishati Mbadala kutoka REA, Mhandisi Advera Mwijage, amesema mradi wa nishati safi ya kupikia katika Shule ya Sekondari ya Wasichana Kondoa umegharimu Shilingi milioni 54.

Amesema katika shule hiyo, limefungwa tanki la gesi lenye ujazo wa tani moja linaloweza kuhudumia upishi kwa takribani miezi miwili, pamoja na mfumo wa mkaa mbadala unaotokana na mabaki ya miwa.

Mkuu wa shule hiyo, Mwl. Flora Nusu, ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita kwa mradi huo, akieleza kuwa utaondoa athari za kiafya kwa wapishi na muda uliokuwa ukipotea katika kutafuta kuni, na pia kupunguza gharama za uendeshaji kwa asilimia 40

Mradi huo ni sehemu ya mpango mkubwa wa kuunganisha miundombinu ya nishati safi ya kupikia katika taasisi 453 wenye thamani ya Shilingi bilioni 25.8, ambapo gharama zote zinagharamiwa kwa asilimia 100 na Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA).




Na Said Mwishehe,Michuzi TV

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Rais Dk.Samia Suluhu Hassan licha ya kukiri uwepo wa changamoto za kiusalama katika Bara la Afrika pia amepongeza jitihada mbalimbali zilizofanywa katika kukabiliana na migogoro.

Dk.Samia pia aligusia mchango uliotolewa na nchi ya Tanzania ambayo ni mchangiaji wa hali na mali pamoja na vijana wake katika kulinda amani barani Afrika.

Akizungumza Ikulu Dar es Salaam alipokuwa akielezea yaliyojiri katika Mkutano wa 39 wa Wakuu wa Nchi na Serikali uliofanyika Addis Ababa nchini Ethiopia , Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mahmoud Thabit Kombo amesema pia katika miaka minne ujumbe wake Rais Dk.Samia Suluhu Hassan katika Baraza Kuu la Usalama na Amani la AU ulihusu masuala yanayosimamiwa na Baraza  ikiwemo uchaguzi, pia Amani na usalama.

“Wakati wa Baraza hilo la Usalama na Amani la AU Rais Dk.samia Suluhu Hassan pia alieleza changamoto zilizotokezea nchini kwake na kuelezea pia jitihada za Serikali yake bila kuhitaji msaada kutoka nje zilizofanywa na Serikali yake kukabiliana na changamoto hizo zilizotokea

“Sisi tunaweza kuona changamoto zetu kubwa sana lakini kule ni kama punje tu ya ngano kwasababu ukichukulia migogoro ya wenzetu ni mikubwa zaidi ,ni mipana zaidi ya miaka mingi,huku kwetu ni kama upepo unaopita,”amesema Waziri Kombo 

Wakati anaeleza hayo Waziri Kombo amesema kwamba “Kama mnavyojua Tanzania imekuwa ni Mjumbe katika Baraza la Usalama na Amani la AU kwa miaka minne mfululizo mara mbili na mwaka 2029 Mungu akijaalia Tanzania itakuwa mjumbe katika Baraza la Usalama na Amani la Umoja wa Mataifa.

Ambapo amesema kwa hivi sasa Tanzania ilianza tokea mwaka 2022 hadi mwaka huu wanapomaliza rasmi kuwa mjumbe wa baraza la usalama na amani Barani Afrika.

“Na ndio  maana sisi ushiriki wetu ulikuwa mkubwa wakati wa vikao vya Baraza hilo la Usalama na Amani kuanzia  mwanzo kwenye ajenda mpaka uwasilishaji kwenye Baraza Kuu.”

Akieleza zaidi pia amesema katika  mkutano wa AU ajenda Kuu ilikuwa hali ya usalama na amani barani Afrika ambapo Waziri Kombo amejulisha kwamba waheshimiwa wakuu wa nchi zote walijikita kujadili ajenda hiyo kwasababu hali ya usalama na amani sio shwari barani Afrika

“Afrika tunapitia  wimbi la mtihani ambalo linatokana na mambo mbalimbali yakiwemo ushindani wa rasilimali zilizokuwepo barani Afrika ambalo kwa sasa linaonekana kwa duniani ndio limebakia kuwa na rasilimali nyingi zaidi kuliko bara lolote lie duniani na hii ni kwa takwimu na kisayani 

“Kwa lugha nyingine utajiri mkubwa uko barani Afrika zaidi kuliko bara lolote,ukichukua utajiri wa maji,rotuba ndani ya aridhi,utajiri wa hali ya hewa ,utajiri wa oksijeni tunayovuta duniani. Kwahiyo utajiri wa kıla aina ,pamoja na afya,mazingira na rasilimali nyingine ikiwemo madini zimekuwa visababishi vya uwepo wa migororo tunayoina kwa nchi za Afrika.”



TUME ya Uchunguzi wa Matukio ya Uvunjifu wa Amani yaliyojitokeza wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025, leo Februari 17, 2026 imekutana na Rais mstaafu wa Jumuiya ya Wanasheria Tanzania (Tanganyika Law Society – TLS), Dkt Edward Hosea.

Mkutano huo wa Tume na Dk Hosea umefanyika katika ukumbi wa Tanganyika uliopo jengo la Benki Kuu ya Tanzania (BoT) mkoani hapa, ikiwa ni sehemu ya juhudi za Tume kukusanya taarifa, maoni na ushauri kutoka kwa viongozi mbalimbali.

Katika mkutano huo hoja zilizojadiliwa zilihusu maeneo ya tathmini ya athari za matukio hayo ndani ya nchi na kimataifa na ushauri wa hatua za kijamii na kisheria zinazochukuliwa ili kuimarisha amani, mshikamano wa kitaifa.

Tume inaendelea kukutana na makundi mbalimbali ikiwemo waathirika wa matukio ya uvunjifu wa amani, kwa lengo la kukusanya ushahidi na taarifa zitakazoiwezesha kuandaa ripoti ya kina.







Viongozi wa vyama vya Wafanyakazi, Waajiri na Shirikisho nchini wametakiwa kuwa mstari wa mbele kuzingatia sheria na katiba za vyama vyao ili kuendelea kuleta ustawi na tija sehemu za kazi pamoja na kukuza ushirikiano na Serikali.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Clement Sangu amesema hayo leo Februari 17, 2026 katika kikao kazi cha Viongozi wa Vyama vya Wafanyakazi, Waajiri na Shirikisho kilichofanyika jengo la PSSSF, jijini Dodoma ambapo alisisitiza kuwa uongozi bora na uwajibikaji unajengwa kwa kuheshimu misingi ya kisheria na taratibu zilizowekwa, hivyo husaidia kuimarisha mahusiano ya kazi na kulinda maslahi ya wafanyakazi pamoja na waajiri.

Aidha, Waziri Sangu amehamasisha viongozi hao kutekekeza Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050 ili kujenga uchumi shindani, jumuishi na kukuza teknolojia. Amesema ili kufikia malengo hayo, ni lazima maeneo ya kazi na soko letu la ajira liwe na utulivu na tija ya hali ya juu ili kuendelea kuongeza ubora wa utoaji huduma na uzalishaji bidhaa zenye ushindani.

Vilevile, Waziri Sangu amesema Serikali itaendelea kuboresha mazingira ya ustawi wa Vyama vya Wafanyakazi na Waajiri ili kuwa na faida ambayo itajenga maslahi bora, usalama wa kijamii na mazingira bora ya kazi.

Akizungumza awali, Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mary Maganga amesema kikao kazi hicho kililenga kuimarisha dhana ya Utatu, ambayo ndiyo nguzo kuu ya amani ya sehemu za kazi na ustawi wa soko la ajira nchini.

Naye, Rais wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA), Tumaini Nyamhokya amesema kuwa shirikisho hilo linaendelea kusimamia maslahi ya wafanyakazi nchini na kukuza tija mahali pa kazi ambapo wataendelea kushirikiana na Serikali na waajili kutatua changamoto zilizopo kwa njia ya mazungumzo.

Kwa upande wake, Mkuu wa Idara ya Utafiti, Sera na Mipango kutoka Chama cha Waajiri Tanzania (ATE), Renatus Mbamilo alisema chama hicho kinaendelea kutekeleza majukumu yake kwa kuzingatia Sheria na Mpango Mkakati wa ATE ambao umejengwa kwa kuakisi Dira ya Maendeleo 2050 pamoja na Mpango wa Kitaifa wa Kazi zenye Staha na kwamba wataendelea kutoa elimu kwa waajiri juu ya taratibu za kazi.

Mwakilishi wa Vyama vilivyo Nje ya TUCTA, Michael Pamagi ameishukuru Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kuwezesha kufanyika kwa kikao kazi hicho ambacho kitasaidia kujenga mfumo imara wa mahusiano kazini unaozingatia haki na wajibu kwa wadau wa utatu.

Kikao kazi hicho cha siku moja kiliitishwa na Waziri Sangu kwa ajili ya kuzungumzia masuala muhimu kwa vyama hivyo na Kuendeleza dhamiria ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan ya kujenga mahusiano chanya baina ya serikali na wadau wa utatu ili kufikia malengo ya kukuza ari ya kazi na utu miongoni mwa wafanyakazi nchini ambapo jumla ya viongozi 150 walishiriki.


-Asema waliotambulishwa ni walioingia kwa mara ya kwanza


Na Said Mwishehe,Michuzi TV


WAZIRI wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mahmoud Thabit Kombo, ametoa ufafanuzi wa kwanini Rais Dk.Samia Suluhu Hassan hakutambulishwa au kuzungumza wakati wa Mkutano wa 39 wa Kawaida wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika (AU),uliofanyika Addis Ababa, Ethiopia

Ufafanuzi wa Waziri Balozi Kombo ameutoa baada ya moja ya mtandao kuandika taarifa ya breaking News kwamba katika hali isiyo ya kawaida na ni aibu Adiss Ababa kiongozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hakutambuliwa wala kuruhusiwa kuzungumza wakati wa ufunguzi wa mkutano wa 39 wa AU.

Akitoa ufafanuzi mbele ya waandishi wa habari Ikulu jijini Dar es Salaam Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mahmoud Thabit Kombo ameeleza kwa kina na hatua kwa hatua kuhusu sababu ambazo zimefanya Rais kutotambulishwa.

“Naomba ndugu zangu (waandishi wa habari) muelimishe jamii kuhusu jambo hili, wakuu wa nchi walioruhusiwa kuzungumza ni wale walioingia mara ya kwanza baada ya Uchaguzi Mkuu katika nchi zao.

“Mh. Rais Dk.Samia Suluhu Hassan amehudumu miaka minne kabla ya Uchaguzi Mkuu kwahiyo kule AU ameshahudhuria mara kadhaa na alishahutubia mara ya kwanza baada ya kifo cha aliyekuwa Rais Dk.John Magufuli.Rais Dk.Samia alihutubia kule…

“Hivyo waliohutubia katika Mkutano wa 39 wa AU ni wale waliongia mara ya kwanza ni zilikuwa nchi tatu ambapo marais wake waliruhusiwa kujitambulisha na kusalimia .Nao ni Gabon ,Ushelisheli na Gine ambao ndio wameingia mara ya kwanza.”

Ameongeza kuwa “ hao walioandika mitandaoni wametafsiri Dk.Samia ameingia AU mara ya kwanza lakini kule ameshazungumza na wanatafsiri miaka minne alikuwepo.

“Kwetu sisi tafsiri yetu sio miaka minne yake kwasababu alıshikilia ule mwaka mmoja Rais kushinda akamalizia ile miaka minne ,kwetu sisi ni mara ya kwanza lakini kule ameshahutubia,”

Katika msisitizo wa ufafanuzi wake Balozi Kombo amesema wakuu wa nchi wale wote waliorudia hawakuzungumza na hivyo sio kwa Rais Samia peke yake bali wako wengi.”Hivyo nimetoa ufafanuzi ili umma ujue sababu yake.”





ZAIDI ya wawekezaji na wafanyabiashara 100 wamehudhuria Semina ya Uwekezaji iliyofanyika leo tarehe 17/2/2026 katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, kwa mafanikio makubwa.

Semina hiyo imewakutanisha wadau mbalimbali wa sekta ya uwekezaji, ambapo washiriki walipata fursa ya kuuliza maswali, kueleza changamoto wanazokutana nazo katika shughuli zao, pamoja na kujifunza na kujadili kwa kina masuala ya uwekezaji na vivutio vinavyotolewa na Serikali kupitia Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalum ya Kiuchumi Tanzania (TISEZA).

Aidha, washiriki walipata ufafanuzi wa kina kuhusu fursa zilizopo mkoani Mbeya na namna bora ya kuzitumia kwa manufaa ya uchumi wa mkoa na Taifa kwa ujumla.

Semina hiyo ilitolewa na Meneja wa Uhamasishaji Uwekezaji wa TISEZA, Bw. Daudi Riganda, ambaye aliwasilisha mada kuhusu vivutio vya uwekezaji, taratibu za usajili, pamoja na faida za kuwekeza kupitia TISEZA.

Mgeni rasmi katika semina hiyo alikuwa Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Beno Malisa, ambaye aliipongeza TISEZA kwa kuendelea kusogeza huduma za uwekezaji karibu na wananchi.

Katika hotuba yake alisema, “Nawashukuru sana TISEZA pamoja na Waziri wa Mipango na Uwekezaji kwa jitihada hizi za kumsaidia Rais kufikia DIRA 2050.

Huu ni mwamko mpya wa sekta binafsi kwa kushirikiana na Serikali kuchangamkia fursa za uwekezaji zilizopo na kusonga mbele katika safari ya maendeleo.”

Semina hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa kampeni ya kitaifa ya kuhamasisha uwekezaji wa ndani, yenye lengo la kuimarisha ushiriki wa sekta binafsi katika kukuza uchumi na kuleta maendeleo endelevu.


Kwa uongozi wa Mganga Mkuu wa Mkoa wa Geita, Dkt. Omar Sukari ( pichani), wadau (ikiwemo GGML, TACAIDS, LGAs, na washirika wengine)  wanaratibu mbinu zitakazokuwa za kijamii, endelevu na zenye matokeo yanayopimika.
Majadiliano ya kimkakati yakiendelea ili kubuni afua mahsusi zitakazowafikia wachimbaji wadogo katika Mkoa wa Geita, kundi lenye changamoto na hatari za kipekee katika mapambano dhidi ya VVU.







*Ili.Kuimarisha Uwajibikaji na Uhakiki wa Kina

Na Mwandishi Wetu
GEITA Gold Mining Limited kupitia mpango wake wa Kilimanjaro Challenge Against HIV and AIDS Trust (Kili Trust) imeandaa warsha ya kuwajengea uwezo wanufaika wake, inayofanyika jijini Mwanza kuanzia Februari 16–20, 2026. Warsha hiyo inawakutanisha wanufaika, wadau wa utekelezaji, washirika na wadhamini kwa lengo la kuimarisha utawala bora, uwajibikaji wa kifedha na kuongeza matokeo chanya ya programu.

Warsha hii ni hatua muhimu ya kiutawala kabla ya utoaji wa fedha kupitia Kili Grants Portfolio ya mwaka 2024/2025, inayolenga kusaidia miradi ya uwezeshaji wa kiuchumi, uimarishaji wa afya za jamii na mipango endelevu. Kupitia mpango huo, jumla ya watu 2,309 wananufaika moja kwa moja na 19,690 kwa njia isiyo ya moja kwa moja katika mikoa sita ya Tanzania.

Kama sehemu ya kuimarisha mfumo wa utawala na uwajibikaji, Kili Trust inazitaka taasisi zote zitakazonufaika kupitia mchakato wa uhakiki wa kina (due diligence), mafunzo elekezi kabla ya kuanza utekelezaji wa miradi, mafunzo ya usimamizi wa ruzuku, usimamizi wa fedha pamoja na ufuatiliaji na tathmini kabla ya kupokea fedha. Hatua hizi zinalenga kuhakikisha fedha zinatumika kwa uwazi, ufanisi na kwa kuzingatia malengo yaliyokusudiwa.

Kili Challenge ilianzishwa mwaka 2002 na Geita Gold Mining Limited na imekua kuwa miongoni mwa mipango mikubwa ya sekta binafsi nchini Tanzania katika mapambano dhidi ya VVU na UKIMWI, kwa kushirikiana na Tume ya Taifa ya Kudhibiti UKIMWI (TACAIDS) ili kuimarisha usimamizi na mwafaka wa kitaalamu.

Akizungumza katika warsha hiyo, Meneja wa Kili Trust, Bw. Stephen Mhando, amesema Kili Challenge ya kila mwaka si tukio la kuchangisha fedha pekee, bali ni wito wa kitaifa wa kuchukua hatua unaowaunganisha washirika, jamii na watu binafsi kusimama pamoja na watu wanaoishi na VVU na UKIMWI. Amesema kupitia rasilimali zinazokusanywa kila mwaka, Trust inaendelea kupanua afua zenye kuleta mabadiliko chanya kwa kuwezesha kiuchumi, kuboresha upatikanaji wa huduma za afya na kupunguza unyanyapaa, ili kuhakikisha matokeo endelevu katika jamii zinazonufaika.

Mwaka huu, programu imepanua wigo kwa kuwajumuisha wachimbaji wadogo kama kundi lenye hatari zaidi ya maambukizi ya VVU kutokana na uhamahama, mazingira yasiyo rasmi ya kazi na upatikanaji mdogo wa huduma za afya. Afua maalum zitalenga kuongeza uelewa, kuimarisha kinga, upimaji, uunganishaji wa matibabu pamoja na kujenga ustahimilivu wa jamii katika maeneo ya uchimbaji.

Kili Challenge inaendelea kufadhili afua mbalimbali zikiwemo uwezeshaji wa kiuchumi kwa watu wanaoishi na VVU, mipango ya usalama wa chakula, huduma za kinga na matibabu zinazotolewa katika jamii, kupunguza unyanyapaa na kutoa msaada wa kisaikolojia, pamoja na kuimarisha mifumo ya afya na mitandao ya rufaa. Kwa kuimarisha uzingatiaji wa masharti, uwazi na matokeo yanayopimika, Trust inalinda imani ya wafadhili na kuhakikisha kila shilingi inayokusanywa inaleta matokeo halisi kwa jamii.

Wakati maandalizi ya Kili Challenge 2026 yakishika kasi, Trust inazihimiza kampuni, taasisi na watu binafsi kushiriki katika kampeni ya mwaka huu ya uchangishaji fedha kwa lengo la kuchangisha Dola za Kimarekani milioni 1 mwaka 2026, ili kuendeleza azma ya Tanzania na UNAIDS ya kutokomeza janga la UKIMWI ifikapo mwaka 2030.

MKUU wa Mkoa wa Dar es salaam Mhe Albert Chalamila amemaliza mgogoro uliodumu kwa takriban miaka 15 katika eneo la kariakoo ukihusisha familia ya marehemu Abdallah Sultani Mtambo akiwemo aliekuwa mkewe Bi Malaya Mtambo na Salim Selemani Salim ambae alinunua nyumba hiyo namba 12 kiwanja namba 15 kupitia mnada wa mahakama ambapo amemkabidhi Salim Selemani Salim kama mmiliki halali alieinunua nyumba hiyo kihalali

Akizungumza leo Feb 17 Jijini Dar es salaam mara baada ya kusikiliza taarifa ya kamati aliyoiunda alipotembelea nyumba hiyo mwezi januari mwaka huu RC Chalamila amesema amejiridhisha kuwa kwa mujibu wa maelekezo ya mahakama nyumba hiyo ni ya Salim Selemani Salim kwani aliinunua kisheria chini ya usimamizi wa mahakama kwa kiasi cha shilingi milioni 250 tangu mwaka 2011

Aidha RC Chalamila amesema baada ya nyumba hiyo kuuzwa kisheria baadhi ya warithi walipokea fedha hizo kutoka kwa dalali wa mahakama lakini baadhi ya warithi akiwemo Bi Malaya waligoma kuchukua fedha hiyo ambapo kiasi cha shilingi milioni 64 na laki tano ambayo hadi sasa ipo kwa dalali huyo hivyo ameelekeza dalali huyo kizikabidhi fedha hizo ziende mahakamani ali zikabidhiwe kwa wahusika kwa kuzingatia taratibu za kimahakama.

Akitoa taarifa ya kamati iliyoundwa na Mkuu wa Mkoa Mwenyekiti wa kamati hiyo ambae pia ni Mwanasheria wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Fabiola Mwingira amesema kamati imefuatilia kwa kina mgogoro huo na kubaini kuwa taratinu zote za kimahakama zilifuatwa baada ya warithi kutoelewana na mahakama kusimamia uuzwaji wa nyumba hiyo

Kwa upande wa Mkuu wa Wilaya ya Ilala Mhe Edward Mpogolo ameshukuru mgogoro kumalizika na kuahidi kushirikiana na kamati yake ya usalama kuhakikisha amani ina imarika mahali hapo. 





Top News