▪️ Asema utekelezaji wa Bwawa la Farkwa kuanza baada ya kukamilika kwa taratibu za manunuzi

▪️ Aagiza kukomeshwa kwa ukamataji usio na msingi wa vitendea kazi vya wananchi

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, amesema Serikali imejipanga kuhakikisha miradi yote ya maendeleo iliyopungua kasi ya utekelezaji inaanza tena kutekelezwa kwa kasi inayotakiwa ili wananchi waendelee kunufaika na huduma za kijamii na kiuchumi.

Amesema hayo leo Jumapili, Mei 17, 2026, alipowahutubia wananchi wa Wilaya ya Chemba katika Viwanja vya Shule ya Msingi Kambi ya Nyasa, akiwa katika ziara ya kusikiliza na kutatua changamoto za wananchi.

Dkt. Mwigulu amesema baadhi ya miradi ilipungua kasi baada ya Serikali kuelekeza nguvu kubwa katika kukamilisha miradi ya kimkakati ya kitaifa iliyokuwa imefikia hatua za mwisho, ikiwemo Mradi wa Kufua Umeme wa Julius Nyerere, reli ya kisasa pamoja na Daraja la Kigongo–Busisi.

“Kilichosababisha baadhi ya miradi kupungua kasi haikuwa uzembe wala kupuuza. Ilikuwa ni mkakati wa kukamilisha miradi iliyokuwa imekaribia kukamilika ili ianze kutumika,” amesema.

Amesema Serikali sasa imeweka kipaumbele katika kuhakikisha miradi yote iliyokuwa imepungua kasi inaanza tena kutekelezwa, huku miradi ambayo mikataba yake tayari imesainiwa ikitengewa fedha za kuanza kazi.

Kuhusu Mradi wa Bwawa la Farkwa, Dkt. Mwigulu amesema mradi huo, unaokadiriwa kugharimu zaidi ya shilingi bilioni 312, utaanza kutekelezwa mara baada ya kukamilika kwa taratibu za kimanunuzi.

“Tunapoanza bajeti mpya naamini mtakuwa mmeanza kuona mkandarasi akiwa eneo la mradi kutekeleza mradi huo wa kihistoria,” amesema.

Amesema Serikali imeelekeza miradi mipya ya maji ibuniwe kwa namna itakayotoa huduma ya maji kwa matumizi ya nyumbani, mifugo na shughuli za kilimo.

Aidha, Dkt. Mwigulu amesema Serikali imeendelea kufanya uwekezaji mkubwa katika sekta za afya, elimu, maji na nishati, hatua ambayo imebadili kwa kiwango kikubwa maisha ya wananchi.

Katika sekta ya afya, amesema Serikali imejenga hospitali za wilaya zaidi ya 100, vituo vya afya zaidi ya 600 na zahanati zaidi ya 2,700, sambamba na ununuzi wa vifaa tiba vya kisasa vya uchunguzi katika hospitali za rufaa na za kanda.

Katika sekta ya elimu, amesema Serikali imejenga shule za amali 103, zikiwemo shule 29 za mkondo wa uhandisi, pamoja na kuendelea kuongeza miundombinu ya shule za msingi na sekondari nchini.

Kuhusu nishati, Dkt. Mwigulu amesema Serikali imejipanga kumaliza changamoto ya kukatika kwa umeme kupitia utekelezaji wa Mradi wa Gridi Imara wenye thamani ya zaidi ya shilingi trilioni 1.1.

“Mkiona umeme unakatika katika baadhi ya maeneo siyo upungufu wa umeme tena. Changamoto ipo kwenye uimara wa gridi kutokana na ongezeko kubwa la matumizi,” amesema.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu ameagiza viongozi na watendaji kuacha vitendo vya ukamataji usio na msingi pamoja na kushikilia vitendea kazi vya wananchi kwa makosa madogo.

“Haya mambo ya kushikilia vitendea kazi vya wananchi tuachane nayo. Mtu anafanya shughuli yake ya kujitafutia kipato halafu mnachukua kitendea kazi chake; hiyo ni kuua mtaji na maisha ya familia yake,” amesema.

Amesema Serikali itaendelea kulinda haki za wananchi na kuhakikisha sheria hazitumiki kuwaonea wananchi au kuwanyima fursa za kufanya shughuli halali za uzalishaji.

Aidha, amesema Serikali inaendelea na hatua za kuifuta sheria ya kutaifisha mali ambayo imekuwa ikitumika vibaya katika baadhi ya maeneo na kusababisha wananchi kupoteza mali zao isivyo halali.








Na Mwandishi wetu – Dar es Salaam

Serikali imeeleza hazma yake ya kuendelea kutekeleza miradi ya mashirikiano katika sekta za kilimo na Uvuvi kwa pande mbili za Muungano ili kuongeza Ajira, uzalishaji mali, kuboresha usalama wa chakula, kuongeza thamani ya mazao, na kukuza Uchumi wa Buluu.

Hayo yameelezwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Bunge, Uratibu na wenye Ulemavu Profesa Palamagamba Kabudi katika kikao cha ngazi ya Mawaziri cha Mashirikiano kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kilichofanyika katika Ukumbi wa Mkutano wa Ofisi ya Waziri Mkuu Mtaa wa Magogoni Jijini Dar es Saalaam leo Tarehe 17 Mei 2026.

Azingumzia Programu ya kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) inayotekelezwa na pande zote Mbili za Muungano, Profesa Kabudi amesema Serikali itaimarisha ushiriki katika sekta ya uvuvi wa Bahari kuu kwa kuwezesha mashirika ya uvuvi (TAFICO) kwa Tanzania Bara na (ZAFICO) kwa upande wa Zanzibar kwa kuwezeshwa kujenga meli sita za uvuvi sambamba na ujenzi wa viwanda vya kuchakata Samaki ambapo kwa upande wa Tanzania Bara kiwanda hicho kitajengwa katika wilaya ya Kilwa Mkoani Lindi na Zanzibar katika eneo la Fungurefu.

Aidha, kwa upande wa Utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi alisema kuwa, Serikali imejiandaa kutoa taarifa ya Utekelezaji wa Ilani ya chama hicho ya nusu mwaka kwa pande zote mbili za Muungano ifikapo mwezi Julai, 2026 na taarifa ya mwaka mzima ifikapo mwezi Novemba 2026.

Kwa upande wake Waziri wa Nchi, Ofisi wa Makamu wa Pili wa Rais anayeshughulikia masuala ya Sera, Uratibu na Baraza la Wawakilishi Mhe. Hamza Hassan Juma alisema Watanzania wengi wanajishughulisha na masuala ya kilimo hivyo kikao hicho kimeweza kuzungumzia fursa zinazopatikana katika sekta hizo zinazoratibiwa na ofisi hizo na kuongeza kuwa mafanikio mengi yanategemewa kupatikana katika vikao hivi vya mashirikiano.












-Ampongeza Rais Samia kuunda Tume kuchunguza kabla na baada ya Uchaguzi Mkuu

MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Tanzania Bara, Stephen Wasira amesema kabla ya kuanza kwa mchakato wa maridhiano ya kisiasa, ni vyema kuwabaini kuwachukulia hatua za kisheria kupitia vyombo vya haki watu waliohusika na vurugu zilizosababisha madhara vikiwamo vifo.

Amempongeza Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kwa kuunda Tume ya Kuchunguza Vurugu za Wakati na Baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025 kwa lengo la kujua kiini cha tatizo hilo.

Wasira lieleza hayo jana alipohutubia mkutano wa hadhara Mjini Kigoma akiwa katika ziara ya kichama mkoani humo.

"Mimi sijasema jina la mtu, lakini wenye kujua hayo mambo wanajijua, waache jinai ichunguzwe kama walihusika waende kwenye vyombo vya haki na sio wengi, wanaobaki watu wema tukae tufanye nao maridhiano," alisema.

Alimpongeza Rais Samia kwa kuunda tume ya kusaidia kujua chanzo cha vurugu hizo, pia alipongeza kazi nzuri iliyofanywa na tume hiyo kufanya uchunguzi huo.

"Rais (Dk. Samia) tunamshukuru na kumpongeza sana, kwa kuunda tume ya kutusaidia kujua chanzo. Tunampongeza na tunaipongeza tume ambayo imesema katika uchunguzi wake imegundua kuna watu si wengi lakini ndio walioanza mpango ule walifadhili.

"Sasa wanasema (tume) wao hawakuwa polisi wa kuwakamata, lakini wanasema tuchunguze wale walioonekana ili tusiwe tunafuga nyoka ndani ya nyumba," alisema.

Alisema hakuna anayeshabikia matukio yenye kuumiza yaliyosababisha vifo na kwamba anayefanya hivyo hayuko sawa kiakili.

"Wanasema watu wamekufa, ni nani anafurahia kufa watu labda uwe na wewe akili yako imeharibika kama unasherehekea kufa watu. Wote tunapinga mauaji, lakini nani amesababisha, halafu wale walioko wengine kama tunawahisihisi ndio tena wanataka kutufundisha namna ya kufanya...vurugu muanzishe nyie na namna ya kumaliza mgogoro mtupe nyie, hapana," alisema.








WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali itaendelea kuhakikisha Mradi wa Maji wa Miji 28 katika Mji wa Chemba unakamilika kwa wakati ili kuongeza upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama kwa wananchi wa Wilaya ya Chemba.

“Wilaya ya Chemba ni moja ya wilaya zenye shida ya ukame na maji, lakini pia ni wilaya za uzalishaji, kwa hiyo tunahitaji sana mradi huu ukamilike haraka,” amesema.

Waziri Mkuu amesema hayo leo Jumapili, Mei 17, 2026 wakati alipotembelea na kukagua maendeleo ya utekelezaji wa Mradi wa Maji wa Miji 28 katika Mji wa Chemba unaotekelezwa kupitia Wizara ya Maji kwa kushirikiana na Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) Wilaya ya Chemba.

Akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa mradi huo, Mkurugenzi wa Usambazaji Maji kutoka Wizara ya Maji, Eng. Charles Mafie amesema mradi huo wenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 11 unatarajiwa kuhudumia wananchi zaidi ya 18,141 wa Mji wa Chemba pamoja na vijiji vya Chemba, Chambalo, Kambi ya Nyasa, Gwandi, Paranga na Makamaka.

Amesema mradi huo umefikia asilimia 76 ya utekelezaji na unahusisha ujenzi wa visima vitatu vyenye uwezo wa kuzalisha maji lita 207,000 kwa saa, matenki ya kuhifadhi maji, kituo cha kusukuma maji pamoja na ulazaji wa mabomba ya kusambaza maji yenye urefu wa kilomita 60.

Aidha, amesema mradi huo utaongeza upatikanaji wa maji kutoka asilimia 37 ya sasa hadi asilimia 100 na kuongeza uzalishaji wa maji kutoka wastani wa lita laki moja na sabini kwa siku hadi kufikia zaidi ya lita milioni tatu kwa siku.

Mradi huo unatekelezwa na Mkandarasi M/s Megha Engineering and Infrastructure Limited (MEIL) chini ya usimamizi wa Mhandisi Mshauri WAPCOS Limited.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amewataka wakandarasi wanaotekeleza mradi huo kuhakikisha wanawalipa kwa wakati vijana, mafundi na vibarua wanaoshiriki katika utekelezaji wa kazi kupitia mikataba ya ushirikiano (subcontracting).

“Muendelee na kazi, lakini kila mnapopata fedha za mradi hakikisheni mnawalipa wanaofanya kazi pamoja nanyi. Vijana wetu waliopata subcontracting, mafundi na vibarua wote wapate malipo yao kwa wakati,” amesema.

Pia amesema Serikali imekuwa ikipokea malalamiko katika baadhi ya maeneo kuhusu miradi kukamilika huku baadhi ya watu waliohusika katika utekelezaji wake wakibaki wanadai malipo yao jambo ambalo halikubaliki.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amesema ana imani kubwa na usimamizi wa viongozi wa Serikali katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo akieleza kuwa usimamizi madhubuti una mchango mkubwa katika kuhakikisha miradi hiyo inaleta matokeo chanya kwa wananchi.






-Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa aridhishwa na miradi ya REA

📍Nyasa - Ruvuma

Wananchi wa Kitongoji cha Ndecha Wilaya ya Nyasa mkoani Ruvuma wameanza kushuhudia mwanga wa matumaini baada ya kuzinduliwa rasmi kwa mradi wa REA kwa gharama ya zaidi ya shilingi bilioni 4.17 wa kusambaza umeme unaotekelezwa kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA), mradi ambao unatarajiwa kuleta mageuzi makubwa ya kiuchumi na kijamii kwa wananchi wa eneo hilo.

Mradi huo umezinduliwa tarehe 16 Mei, 2026 na Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa, Ndugu  Wazo Michael Mwang’onda, ambaye amesema kuwa dhamira ya Serikali ni kuhakikisha wananchi wa vijijini wanapata huduma bora za nishati ili kuboresha maisha yao na kuchochea maendeleo ya Taifa.

Halikadhalika Bw. Mwang'onda  amewataka wananchi kutumia nafasi hiyo ya mradi kulipa shilingi 27,000 tu ili waweze kuwekewa umeme huo. 

“Tunataka kuona wananchi wanalipia 27,000 ili wawekewe umeme hata ukiuza kuku mmoja 27,000 unaenda kuweka umeme kwenye nyumba yako sio 300,000 kama ilivyokuwa hapo zamani'' amesema Kiongozi wa Mwenge kitaifa. 

Kwa upande wake, Msimamizi wa Miradi ya REA Mkoa wa Ruvuma, Mha. Hamisi  Mrope, amesema mradi wa kusambaza umeme vijijini (REDP2C) katika Wilaya ya Nyasa unalenga kufikisha huduma ya umeme katika vitongoji vyote ili kuinua maisha ya wananchi na kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

Aidha, Mha. Mrope amesema mradi huo ulianza rasmi tarehe 16 Novemba 2023 na unatarajiwa kukamilika  ifikapo mwezi Oktoba, 2026, huku ukihusisha vitongoji 30, mashine umba 30 pamoja na wateja 1,247 kwa gharama ya zaidi ya shilingi bilioni 4.17.

Katika Kitongoji cha Ndecha pekee, mradi umehusisha ujenzi wa kilomita 8.43 za njia ya umeme, ufungaji wa mashine umba mbili pamoja na kuunganisha wateja 94 kwa gharama ya zaidi ya shilingi milioni 307.6. Hadi sasa, miundombinu imekamilika kwa asilimia 100 huku wananchi 56 tayari wakiwa wameunganishiwa huduma ya umeme kwa gharama nafuu ya shilingi 27,000 kwa kila mteja.

Mradi huo unatekelezwa na Mkandarasi mzawa MF Electrical Engineering Ltd chini ya usimamizi wa TANESCO.

Naye, Mbunge wa jimbo  la Nyasa Mhe. John Nchimbi amesema miradi ya REA imesaidia kwa sasa vijiji vyote 84 vya wilaya Nyasa kupata huduma ya umeme huku Tanzana ikijivunia kuwa ya pili Afrika Mashariki kwa kusambaza umeme.

Kwa upande wake, Mkandarasi wa mradi huo MF Electrical Engineering Ltd mhandisi Mussa David amesema mradi huo kwa kitongoji cha Ndecha 1 wameshafikisha umeme na wameshawasha nyumba 56.

Wananchi wa Ndecha wameeleza furaha yao kutokana na ujio wa umeme ambapo mwenyekiti wa kijiji cha Linda Antony Nkoma amesema  sasa wataweza kufanya shughuli zao za kiuchumi kwa ufanisi zaidi tofauti na zamani walipotegemea taa za vibatari na vyanzo vya nishati visivyo salama.

Uzinduzi wa mradi huo umeonekana kuwa hatua muhimu katika safari ya kuwaletea wananchi maendeleo endelevu huku ukiunga mkono kaulimbiu ya Mwenge wa Uhuru 2026 isemayo:

“Tanzania ni Yetu Sote, Tushikamane kwa Pamoja Kuleta Maendeleo.”







-Wananchi kuvuna lita bilioni 21 za maji chini ya ardhi


Na Mwandishi wetu


UTAFITI uliofanywa na Bodi ya Maji ya Wami Ruvu (WRWB) umeonesha kuwepo wa maji lita bilioni 21 za maji chini ya ardhi zitakazotumika kama mbadala wakati wa kipindi cha ukosefu wa maji katika mikoa ya Dar es Salaam na Pwani.

Hatua hiyo muhimu ya WRWB ni sehemu ya utekelezaji wa awamu ya kwanza katika kutafuta vyanzo vipya mbadala vya maji katika kukabiliana na ukosefu wa mji katika mikoa ya Dar es salaam na Pwani.

Utekelezaji wa uchimbaji wa visima virefu vya maji

mbadala (back up) unatekelezwa na WRWB kwa awamu mbalimbali katika jiji la Dar es salaam na Mkoa wa Pwani kama mbadala wa maji hii ni kutokana na kuwepo kwa vipindi vya ukame jambo ambalo limekuwa likiathiri uvunaji maji katika bonde na kusababisha mgao wa maji katika maeneo ya Pwani na Dar es salaam

Aidha, uchimbaji wa awamu ya kwanza unatarajiwa kukamilika mwishoni mwa Juni 2026.

Kwa mujibu wa mtaalam wa haidrojia kutoka WRWB,Omary Kizulwa alisema bodi imeamua kuwatumia wataalamu wake ili kubaini vyanzo vipya vya maji ili kuondoa kero ya maji katika mikoa ya Pwani na Dar es Salam kwa kuchimba visima mbadala vya kuhifadhi maji katika maeneo mbalimbali.

“Kwa sasa hivi Bodi ya Maji Bonde la Wami Ruvu tunafanya tafiti katika jiji la Dar es salaam na Pwani tafiti hizi zinatuwezesha kubaini maeneo ambayo yana vyanzo vya maji chini ya ardhi ili tuweze kuchimba visima” “Visima hivi vitakua kama back up (mbadala) kusaidia kipindi ambapo ukame unapotokea au ambapo hata ukame hamna viweze kutumika katika kutoa huduma ya maji” alisema“Zoezi la utafiti na uchimbaji linaendelea mpaka sasa tumeshafanya utafiti zaidi ya maeneo 40, Maeneo ya Ruvu Juu, Ruvu chini, Kigamboni , Chamazi, Ubungo, Kinondoni na Mburahati” alisema

“Tumeshafanya tafiti na tumeshaweka pointi na hivi sasa tunavyozungumza mitambo ipo site inaendelea na uchimbaji mpaka sasa zaidi ya visima 17 vimechimbwa na baadhi ya visima vimeonesha uwezo mkubwa kutoa maji na ni maji mazuri, mfano eneo la Mburahati tumechimba kisima kikubwa pale kina uwezo wa kutoa maji takribani lita elfu 50,000 mpaka 100,000 kwa saa na visima vingine kama Ilala na visima vya huku Chamazi vina karibia elfu 10,000 mpaka elfu 20,000 na kuendelea”

Aidha mtaalam huyo alisema kuwa Tanzania haina uhaba wa maji huku akibainisha kuwa maji chini ya ardhi ni lita bilioni 21 na maji juu ya ardhi ni lita bilioni 105

MRADI WA KIDUNDA

Aligusia pia mradi wa maji wa kimkakati wa Bwawa la Maji Kidunda unaotekelezwa kwa gharama ya sh.bilioni 336 kuwa utasaidia nao kuhifadhi maji ya juu ya ardhi kipindi ambapo kuna ukame

Kwa mujibu wa serikali Mradi wa Bwawa la Kidunda ni muhimu kwa kuwa utawezesha kukidhi mahitaji ya maji kwa wananchi wanaotarajiwa kuongezeka na kufikianidadi ya watu 11,387,753 ifikapo mwaka 2032, ambapo mahitaji ya maji yanakadiriwa kufikia zaidi ya lita bilioni

1.028 kwa siku. Mradi huo unatekelezwa na Mkandarasi kutoka kampuni ya Sino Hydro Corporation ya nchini China.

Bwawa la Kidunda, litakalokuwa na ujazo wa lita bilioni 190, litawezesha mitambo ya Ruvu Juu na Ruvu Chini, yenye uwezo wa kuzalisha jumla ya lita milioni 466 kwa siku, kufanya kazi katika majira yote ya mwaka na hivyo kuondoa upungufu wa maji wakati wa kiangazi.

Mitambo hiyo inahudumia zaidi ya asilimia 80 ya eneo lote la huduma la DAWASA.

Kwa upande wake wakati wa ziara ya kukagua mradi wa Kidunda msishoni mwa mwaka jana Waziri wa Maji Jumaa Aweso alisema nchi nyingi duniani kwa sasa zinakabiliwa na changamoto ya ukameinayosababishwa na mabadiliko ya tabianchi, hali ambayo pia imeanza kuathiri Tanzania.

Kutokana na hali hiyo, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, aliielekeza Wizara ya Maji kuchukua hatua za haraka na za muda mrefu ili kukabiliana na changamoto hiyo.

“Wizara ya Maji tuliweka mkakati wa muda mfupi jijini Dar es Salaam kwa kuchimba visima vitanovilivyogharimu takribani Sh.bilioni 23.6, sanjari na mkakati wa muda mrefu wa ujenzi wa Bwawa la Kidunda mkoani Morogoro pamoja na mpango wa kutumia maji ya Mto Rufiji mkoani Pwani ili kuongeza uzalishaji wa maji,” alisema

Alisema kwa sasa mahitaji ya maji kwa Jiji la Dar es Salaam ni takribani lita milioni 534 kwa siku, ilhali changamoto ya ukame ikiathiri kwa kiasi kikubwa upatikanaji wa huduma ya maji.



Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Yahya Ramadhan Kido amesema Mkoa wa Kagera unaendelea kufanya vizuri katika uzalishaji wa zao la kahawa, huku akibainisha kuwa hadi sasa mkoa huo una jumla ya miche ya kahawa milioni 85 inayotarajiwa kuongeza tija na kuinua uchumi wa wakulima.

Kanali Kido amesema hayo wakati akifungua mkutano wa wadau wa kahawa mkoani Kagera, ambapo ameeleza kuwa Serikali kupitia ushirikiano na wadau mbalimbali imeendelea kusambaza miche ya kahawa kwa wananchi, huku miche milioni 36.75 ikiwa tayari imetolewa kwa wakulima kwa lengo la kuongeza uzalishaji wa zao hilo muhimu la biashara.

Amesema katika msimu wa 2025/2026 pekee, miche milioni 13.7 ilisambazwa kwa wakulima kupitia ushirikiano kati ya Bodi ya Kahawa Tanzania, halmashauri, vikundi vya wakulima pamoja na sekta binafsi.

Aidha, ameitaka Bodi ya Kahawa Tanzania kuendelea kusambaza miche zaidi kwa wakulima pamoja na kusaidia kutatua changamoto mbalimbali zinazoikabili sekta hiyo, hususan wadudu waharibifu aina ya bungua mweusi ambao wamekuwa wakisababisha hasara kwa baadhi ya wakulima.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Kahawa Tanzania, Primus Kimaryo amesema bado kuna haja kubwa ya kuendelea kutoa elimu kwa wakulima na wafanyabiashara wa zao hilo ili kudhibiti biashara ya kahawa inayofanyika kwa njia za magendo.

Amesema baadhi ya watu wanaojihusisha na biashara hiyo haramu wanatoka ndani ya jamii husika, hali inayochangia upotevu wa mapato kwa wakulima pamoja na Taifa kwa ujumla.

Aidha, Primus Kimaryo amewataka wafanyabiashara kuachana na vitendo vya kuuza kahawa kwa njia zisizo rasmi, huku akiwataka wakulima kuwa waaminifu kwa kuuza kahawa kupitia mifumo halali ili waweze kunufaika zaidi kiuchumi.

Katika hatua nyingine, amesema Mkoa wa Kagera umeendelea kufanya vizuri katika uzalishaji wa kahawa, ambapo uzalishaji wa kahawa ya maganda umefikia zaidi ya tani elfu 50, hatua inayodhihirisha ukuaji wa sekta hiyo ndani ya mkoa huo.





WAZIRI MKUU, amewahimiza wananchi kuendelea kuiombea Tanzania ili amani, umoja na mshikamano wa kitaifa viendelee kuimarika sambamba na nchi kuendelea kupiga hatua za maendeleo katika sekta mbalimbali za kijamii na kiuchumi.

Amesema hayo leo Jumapili, Mei 17, 2026 aliposhiriki ibada katika (KKKT) Usharika wa Kondoa Mjini, Jimbo la Kondoa, Dayosisi ya Dodoma.

Ibada hiyo iliongozwa na Msaidizi wa Askofu wa Dayosisi ya Dodoma, pamoja na Mchungaji Kiongozi wa Usharika wa Kondoa Mjini na Mkuu wa Jimbo la Kondoa KKKT, .

Waziri Mkuu amesema anaendelea kushirikiana na taasisi za dini nchini akitambua mchango wake katika kujenga jamii yenye maadili, umoja na maendeleo.

“Ujumbe wake kwa wananchi wa Kondoa ni kwamba tuendelee kuiombea nchi yetu ili iendelee kuwa ya amani na kuendelea kupiga hatua za maendeleo,” amesema.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amesema Serikali itaendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo iliyopo kwenye Ilani ya Uchaguzi ikiwemo ujenzi wa daraja la kuingia Kondoa Mjini pamoja na daraja la barabara ya kuelekea Hanang.

“Tumebeba jambo la daraja la kuingia hapa Kondoa Mjini, hilo tutaanza nalo. Lakini la pili ni daraja la kuelekea Hanang ambalo na lenyewe kero yake ni kubwa sana,” amesema.

Aidha, Waziri Mkuu amesema Serikali inaendelea na maandalizi ya utekelezaji wa mfumo wa elimu ya lazima wa miaka 10 unaotarajiwa kuanza mwaka 2028.

“Hatutakuwa na jambo linaloitwa mtoto amemaliza darasa la saba. Tunaenda kuondoa mfumo wa kuishia darasa la saba ili elimu ya lazima iwe miaka 10,” amesema.

Amesema utekelezaji wa mfumo huo unahitaji ushiriki na hamasa kutoka kwa Watanzania wote kutokana na umuhimu wa mabadiliko hayo katika sekta ya elimu nchini.

Kwa upande wake, ameishukuru Serikali kwa kuendelea kushirikiana na taasisi za dini nchini.

“Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu , kwa ushirikiano na sisi watu wa imani na viongozi wa dini,” amesema.

Aidha, amesema kanisa linaendelea kumuombea Waziri Mkuu pamoja na viongozi wa Serikali ili waendelee kulitumikia taifa kwa hekima na uadilifu.









Katika bajeti ya Wizara ya Maliasili na Utalii, makabila ya Wadatoga na Wahadzabe ambayo ni sehemu ya Jiopaki ya Ngorongoro Lengai walitia nakshi na uturi bajeti  hiyo kwa kumsindikiza waziri wa Maliasili na Utalii  Dkt.Ashatu Kijaji (Mb) kuingia katika ukumbi wa bunge jijini Dodoma.

Wadatoga ni waumini wa kuoa mke zaidi ya mmoja wanaotokana na jamii yao, wana uwezo wa kuoa hadi wake kumi  na kila mke akafurahia utamu wa ndoa kutoka kwa mume wake. 

Kwa Jamii hii kuwa na wake wengi si heshima tu bali unachukuliwa kama uchumi kwa kuwa utapata watoto wengi watakaokusaidia shughuli za kuchunga mifugo, kulima chakula cha familia, kufanya kazi za uhunzi, kujenga maboma ya familia na kutanua ukubwa wa jina la ukoo.

Wadatoga hawaishiwi "Power" kwasababu hawali chipsi mayai, soseji wala Baga, hawatafuti energy wala dawa za Congo,hawana mawazo ya vikoba,ni mwendo wa vyakula vya asili tu kama Ugali, mtama, ulezi, Maharage, mbaazi, viazi vitamu na Maziwa ambapo mafuta ya kupikia hawanunui dukani bali yanatokana na samli  kutoka kwenye maziwa ya Ng'ombe yaliyogandishwa kisha kuchekechwa kwenye kibuyu maalum na kuzalisha mafuta ambayo husafishwa kiasili na kukaa muda  mrefu bila kuharibika.

Kama wewe ni kijana na unataka kuwa na uwezo wa kuwa na wake wengi karibu makumbusho ya Urithi Jiopaki ujue siri ya wadatoga na vyakula vyao vya miaka na mikaka.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi ameshiriki mazishi ya Marehemu Boniface Makene, aliyewahi kuwa Mwandishi wa Habari wa Makamu wa Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Mohamed Gharib Bilal, yaliyofanyika katika Kijiji cha Mabui Merafuru – Musoma mkoani Mara.

Akitoa salamu za rambirambi kwa waombolezaji, mara baada ya Ibada ya Mazishi iliyofanyika Kanisa Katoliki Parokia ya Mtakatifu Agustino Kijiji cha Mabui Merafuru, Makamu wa Rais ametoa pole kwa familia na kwa waombolezaji wote walioguswa na msiba huo.

Amesema Marehemu Boniface Makene atakumbukwa kwa kuwa mshauri mzuri ambaye aliweza kushauri kwa usahihi na kwa nia njema bila kujali mapokeo ya ushauri huo.

Amesema ni muhimu kuwa na Watanzania wengi wa namna hiyo ambao wanakuwa huru kutoa mawazo yao kwa nia njema, bila kuficha ukweli. Amesema uwepo wa utaratibu wa kuwa wakweli na kutoa mawazo kwa nia njema utawezesha kuijenga nchi kwa kiwango kikubwa sana. Makamu wa Rais amesema ni muhimu kila Mtanzania aone anayo nafasi ya kutoa mawazo yake kwa nia njema ya kuijenga nchi.

Halikadhalika, Makamu wa Rais amewashukuru na kuwapongeza Watanzania waishio nje ya nchi yaani Diaspora kwa kazi kubwa waliyofanya kuhakikisha mwili wa Boniface Makene unarejeshwa nyumbani Tanzania. Amewasihi kuendelea kupendana na kushirikiana pamoja na kukumbushana kwamba Taifa lao ni Tanzania. Makamu wa Rais amesema ni furaha kuona jamii ya Diaspora inapofanya mambo mazuri hususani mmoja wao anapopatwa na changamoto.

Awali akitoa mahubiri wakati wa Ibada ya Mazishi, Paroko wa Parokia ya Mtakatifu Agustino - Mabui Merafuru, Padre Peter Maraga amesema ni vema wanadamu kutumia vipawa walivyopewa na Mungu katika kuwatumikia wanadamu wenzao kama alivyofanya marehemu Makene.

Aidha Padre Maraga, amewasilisha Salamu za Askofu wa Jimbo Katoliki Bunda Mhashamu Simon Masondole ambaye amemkaribisha Makamu wa Rais katika Jimbo hilo na kuahidi kuendelea kumuombea ili kuwa na hofu ya Mungu pamoja na kutimiza majukumu yake kikamilifu.















Top News