Katika juhudi za kutoa ajira na kuinua uchumi wa vijijini, Halmashauri ya Wilaya ya Bukombe imefanikiwa kuuwezesha mradi wa Uuzaji wa Maziwa ya Ng’ombe katika Kijiji cha Msasa, Kata ya Runzewe Magharibi.

Mradi huu unaendeshwa na Kikundi cha MAZIWA BORA-MSASA kilichoanzishwa mwaka 2021 na wanachama 5: Wanaume 2 na Wanawake 3. Baada ya kuona bidii yao, Oktoba 2025 Halmashauri ilikifanyia usajili rasmi

Katika mwaka wa fedha 2025/2026, Halmashauri ilitumia asilimia 10 ya mapato ya ndani kutoa mkopo wa Tsh. 15,000,000/= kwa kikundi hiki kwa kipindi cha miaka miwili.

Hii ni sehemu ya mkakati wa serikali kuhakikisha fedha za wananchi zinawagusa moja kwa moja.

Ili mradi uwe na nguvu zaidi, *Shirika la Heifer International liliunga mkono kwa kutoa ruzuku ya Tsh. 27,807,500

Hivyo kufanya thamani kamili ya mradi kuwa ni Tsh. 42,807,500.

Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Bukombe bi Adelina Mfikwa amesema kuwa halmashauri inaendelea kukipatia kikundi hicho mafunzo mbalimbali ili kiweze kuongeza uzalishaji na bidhaa nnyingi zinatokana na maziwa.

Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Geita Nicholaus Kasendamila ameipongeza halmashauri ya wilaya ya Mbogwe kwa namna inavyowajalu wananchi wake hususani katika mikopo ya vikundi.









Na. Asia Singano, WF- TCHAD

Serikali ya Tanzania imedhamiria kuhakikisha kuwa Wananchi wa Tanzania wanapata huduma za msingi za maji safi na salama kwakuwa maji ni kichocheo muhimu cha mabadiliko ya uchumi na ni muhimu kwa ufanisi wa kilimo, viwanda, uzalishaji wa nishati, maendeleo ya miji, afya ya umma, na ustahimilivu wa tabianchi.

Hayo yalielezwa na Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula (Mb), wakati wa Jukwaa la Maji barani Afrika lenye kaulimbiu, (African Water Forum; from vision to action), linaloendelea kufanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Hoteli ya Radisson mjini N’Djamena, nchini Tchad, alipoongoza Ujumbe wa Tanzania, kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb).

Alisema kupitia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, ambayo utekelezaji wake ulianza tarehe 1 Julai 2026 pamoja na Mpango wa Maji wa Rais, wa Maji na Usafi wa Mazingira (Presidential WASH Compact) unaotarajia kuzinduliwa hivi karibuni, Serikali inalenga kuwaleta pamoja taasisi mbalimbali za Serikali, wadau wa maendeleo, sekta binafsi na jamii kupanua upatikanaji wa maji na usafi wa mazingira, na kukuza uvumbuzi wa kidijitali katika sekta ya maji.

‘’Tumejizatiti kuhakikisha kila kijiji nchini kinapata huduma za msingi za maji safi kufikia mwaka 2031. Hivyo basi, tunasonga mbele na mpango wa uwekezaji wa kimaendeleo utakaounganisha maji kati ya maeneo yasiyo na maji na yale yasiyotoshelezwa” alisema Mhe. Luswetula (Mb).

Alisema kuwa Serikali inatambua umuhimu wa ushirikiano kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP), katika kutekeleza miradi ya maendeleo na kuboresha huduma kwa wananchi huku akizisihi sekta hizo kuendelea kuunga mkono juhudi za Serikali kuhakikisha upatikanaji wa huduma bora kwa wananchi.

‘’Naomba nitoe mwaliko kwa sekta binafsi kushirikiana na Serikali ya Tanzania katika kubadilisha sekta yetu ya maji, fursa kubwa zipo katika uwekezaji wa kimkakati kama vile Gridi ya Taifa ya Maji, huduma za WASH zenye kustahimili mabadiliko ya tabianchi, mifumo ya umwagiliaji, matumizi ya kidijitali kwenye sekta ya maji, na utunzaji wa vyanzo vya maji’’ alisema Mhe. Luswetula (Mb).

Alieleza kuwa Serikali ya Tanzania chini ya Uongozi wa Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, inaendelea kuimarisha mazingira yanayowezesha kuvutia uwekezaji wa muda mrefu, kuweka taratibu za uwazi, sera zinazoweza kutabirika, utawala bora, ili kuyafikia malengo yaliyowekwa kwenye Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Idara ya Maji, Benki ya Dunia (WB), Afrika, Bw. Saroj Kumar, aliipongeza Tanzania kwa kuwa na mikakati bora ya kuboresha maisha ya wananchi, kuandaa na kuanza kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 ambayo imeipa sekta binafsi nafasi ya kuchangia asilimia 70 katika maendeleo ya nchi.

Aliongeza kuwa Benki ya Dunia (WB), inatambua juhudi za Tanzania katika kuendelea kuboresha maisha ya wananchi ambapo juhudi hizo zimejidhihirisha katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 huku Benki hiyo ikiahidi kuendelea kushirikiana na Tanzania katika utekelezaji wa Dira hiyo.

Naibu Waziri wa Fedha, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Laurent Deogratius Luswetula (Mb), (kushoto), akiagana na Mkurugenzi wa Idara ya Maji, Benki ya Dunia (WB), Afrika, Bw. Saroj Kumar, baada ya kuzungumza kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), kwanye Jukwaa la Maji barani Afrika, lenye kaulimbiu "African Water Forum: From Vision to Action", linaloendelea kufanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Hoteli ya Radsson, mjini N’Djamena, nchini Tchad, alipoongoza Ujumbe wa Tanzania, kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb).

Naibu Waziri wa Fedha, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Laurent Deogratius Luswetula (Mb), akifuatilia mijadala mbalimbali wakati wa Jukwaa la Maji barani Afrika, lenye kaulimbiu ‘’African Water Forum; from vision to action, linaloendelea kufanyika katika Ukumbi wa mikutano wa Hoteli ya Radsson, mjini N’Djamena, nchini Tchad, alipoongoza Ujumbe wa Tanzania, kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb).

Naibu Waziri wa Fedha, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Laurent Deogratius Luswetula (Mb), akizungumza wakati wa Jukwaa la Maji barani Afrika, (African Water Forum; from vision to action), linaloendelea kufanyika mjini N’Djamena, nchini Tchad, alipoongoza Ujumbe wa Tanzania, kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb).

Naibu Waziri wa Fedha, Tanzania, Mhe. Laurent Deogratius Luswetula (Mb), (wa tatu kulia), akiwa katika picha ya pamoja na Naibu Waziri wa Maji, Mhe. Mhandisi Kundo Mathew (Mb), (wa tatu kushoto), Kamishna Msaidizi, Idara ya Fedha za Nje, Wizara ya Fedha, Bw. Melckzedek Mbise, (wapili, kulia), pamoja na watumishi wengine kutoka Wizara ya Maji Tanzania, mara baada ya kumalizika kikao cha pili, cha Jukwaa la Maji barani Afrika, lenye kaulimbiu "African Water Forum: From Vision to Action", linaloendelea kufanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Hoteli ya Radsson, mjini N’Djamena, nchini Tchad.


Ujumbe wa Tanzania ukimsikiliza Naibu Waziri wa Fedha, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Laurent Deogratius Luswetula (Mb), (hayupo pichani), alipokuwa akizungumza kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omari (Mb), wakati wa Jukwaa la Maji barani Afrika, lenye kaulimbiu ‘’African Water Forum; from vision to action, linaloendelea kufanyika katika Ukumbi wa mikutano wa Hoteli ya Radsson, mjini N’Djamena, nchini Tchad.

(Picha na Kitengo Cha Mawasiliano Serikalini, WF - Tchad)

Na Paul Kayanda, Kahama


MWENYEKITI wa Mtaa wa Mwime, Manispaa ya Kahama mkoani Shinyanga, Stella Bhayugile, amesema utekelezaji wa miradi ya maendeleo pamoja na mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na Serikali inayoongozwa na Rais Dk Samia Suluhu Hassan umeendelea kuleta matumaini mapya kwa wananchi.

Huku vijana na wanawake wakinufaika kwa kiwango kikubwa kupitia vikundi vyao vya uzalishaji na ujasiriamali.

Akizungumza katika mahojiano maalumu ofisini kwake Jumatano, Julai 15, 2026, Bhayugile alisema Mtaa wa Mwime unaendelea kushuhudia maendeleo makubwa yanayochochewa na usimamizi mzuri wa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Alisema kupitia Halmashauri ya Manispaa ya Kahama, vikundi zaidi ya 12 vya vijana na wanawake katika mtaa wa Mwime tayari vimepatiwa mikopo inayotokana na asilimia 10 ya mapato ya ndani ya halmashauri, hatua ambayo imewawezesha kuanzisha na kupanua shughuli mbalimbali za kiuchumi.

"Mpaka sasa zaidi ya vikundi 12 vya vijana na wanawake vimepata mikopo katika kipindi cha robo mbili za mwaka wa fedha. Mikopo hii imewapa uwezo wa kujiajiri, kuongeza kipato cha familia na kuboresha maisha yao.

Tunamshukuru sana Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuweka mazingira yanayowainua wananchi kiuchumi," alisema Bhayugile.

Alibainisha uongozi wa mtaa huo umeendelea kushirikiana kwa karibu na wananchi katika kusimamia miradi ya maendeleo ili kuhakikisha fedha zinazotolewa na Serikali zinatumika kwa ufanisi na kuleta matokeo yanayoonekana.

Mbali na mikopo hiyo, Bhayugile alisema Mtaa wa Mwime umefanikiwa kujenga zahanati inayotoa huduma za afya kwa wananchi, hivyo kupunguza adha ya kusafiri umbali mrefu kufuata matibabu.

Aidha, alisema eneo hilo lina shule ya msingi yenye wanafunzi zaidi ya 1,886, huku juhudi zikiendelea kuboresha mazingira ya kujifunzia kupitia ujenzi na ukarabati wa miundombinu ya elimu.

Alieleza matundu 16 ya vyoo yamejengwa, na kwa sasa unaendelea mradi wa kufumua mfumo wa mashimo ya zamani ili kujenga vyoo vipya vya kisasa vitakavyokidhi mahitaji ya wanafunzi na walimu.

Katika sekta ya miundombinu, Bhayugile alisema Serikali imetoa zaidi ya Sh milioni 15 kwa ajili ya ukarabati wa barabara za Mtaa wa Mwime na maeneo jirani, hatua ambayo imeboresha usafiri na kurahisisha shughuli za kiuchumi kwa wananchi.

Pia alisema Serikali inaendelea kuwekeza katika kuboresha huduma za elimu kwa watoto wenye mahitaji maalumu, wakiwemo wenye ulemavu wa kusikia, uoni hafifu,mtindio wa ubongo na makundi mengine yanayohitaji mazingira rafiki ya kujifunzia.

Bhayugile alisema mafanikio hayo yametokana na ushirikiano mkubwa uliopo kati ya wananchi, viongozi wa Serikali za Mitaa na Halmashauri ya Manispaa ya Kahama, akisisitiza kuwa maendeleo haya ni ishara ya dhamira ya Serikali ya kuhakikisha hakuna mwananchi anayebaki nyuma.

Aliwataka wananchi kuendelea kushiriki katika shughuli za maendeleo, kulinda miradi inayotekelezwa na kutumia ipasavyo fursa zinazotolewa na Serikali kwa ajili ya kuinua uchumi wa familia na Taifa kwa ujumla.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt.Samia Suluhu Hassan


Na Farida Mangube 

Mbunge wa Jimbo la Ulanga, Salim Alaudin Hashim, ameiomba Serikali kuharakisha ujenzi wa kipande cha barabara ya Lupiro–Mahenge, akisema ni muhimu kwa usafirishaji wa mazao ya kilimo na madini katika Wilaya za Ulanga na Malinyi, Mkoa wa Morogoro.

Ametoa ombi hilo wakati wa hafla ya kumkabidhi mkandarasi kazi ya ujenzi wa Daraja la Namuhanga lililopo Tarafa ya Lupiro. Daraja hilo lilisombwa na mafuriko, jambo lililosababisha usumbufu mkubwa kwa wananchi wa Wilaya za Ulanga na Malinyi.

Mbunge Salim amesema ana imani ujenzi wa daraja hilo utakamilika kwa wakati kabla ya kuanza kwa msimu ujao wa mvua, ili kurahisisha shughuli za kiuchumi, hasa kilimo ambacho ndicho tegemeo kuu la wananchi wa maeneo hayo.

«“Tunashukuru sana Serikali kwa kutuona sisi wananchi wa Wilaya za Ulanga na Malinyi. Wananchi sasa wanaenda kuondokana na adha iliyokuwa ikiwapata kutokana na kusombwa kwa Daraja la Namuhanga,” amesema Mbunge Salim.»

Kwa upande wake, Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega, amesema Mkoa wa Morogoro ni miongoni mwa maeneo yenye changamoto kubwa za miundombinu ya barabara na madaraja, lakini Serikali imejipanga kuhakikisha changamoto hizo zinapatiwa ufumbuzi.

Akizungumzia mradi wa barabara ya Lupiro–Malinyi, Waziri Ulega amesema tayari fedha za ujenzi kwa kiwango cha lami zimetengwa na mkandarasi anatarajiwa kuanza kulipwa malipo ya awali wakati wowote ili kazi ianze rasmi.

"Nyinyi wakazi wa Wilaya hizi mbili ni wazalishaji wakuu wa chakula hapa nchini. Serikali imedhamiria kuhakikisha tunamaliza tatizo hili la miundombinu, hasa barabara ambazo zitajengwa kwa kiwango cha lami ili kuwaondolea changamoto za usafiri na usafirishaji,” amesema Waziri Ulega."

Ujenzi wa barabara na madaraja katika eneo hilo unatarajiwa kuongeza urahisi wa usafirishaji wa mazao, kuchochea biashara na kuimarisha maendeleo ya kiuchumi kwa wananchi wa Ulanga na Malinyi.



Mkuu wa Wilaya ya Morogoro, Mhe. Mussa Kilakala, ameipongeza Wizara ya Nishati kwa kuandaa Warsha ya Nishati Safi ya Kupikia kwa wanahabari na Maafisa habari, akisema mafunzo hayo ni hatua muhimu ya kuhakikisha elimu sahihi inawafikia wananchi na kuimarisha utekelezaji wa ajenda ya matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini.

Akizungumza Julai 14, 2026 wakati wa ufunguzi wa Warsha ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari, Maafisa Mawasiliano Serikalini wa Mikoa, Taasisi, Wizara pamoja na Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Nishati kuhusu uandishi na uhamasishaji wa masuala ya nishati safi ya kupikia inayofanyika katika Ukumbi wa Morena Hotel mkoani Morogoro amesema Mkoa wa Morogoro una vyanzo vingi vya maji vinavyopaswa kulindwa, hivyo ajenda ya kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia itasaidia kuhifadhi mazingira kwa kupunguza ukataji wa miti, kulinda afya za wananchi pamoja na kutunza vyanzo hivyo vya maji kwa manufaa ya kizazinkijacho.

Amesema elimu inayotolewa kupitia warsha hii ikiwafikia wananchi kwa usahihi, itasaidia kuongeza uelewa kuhusu maana na faida za nishati safi ya kupikia, hususan kwa jamii za vijijini, jambo litakalowezesha wananchi kushiriki kikamilifu katika juhudi za kulinda mazingira na kutumia nishati salama na nafuu.

Mhe. Kilakala amewataka washiriki kutoka Mikoa mbalimbali nchini kutumia maarifa waliyoyapata katika warsha hiyo kwa weledi mkubwa wanaporejea kwenye maeneo yao ya kazi kwani mafunzo haya yataongeza hamasa na kuhakikisha wananchi wengi zaidi wanafikiwa na elimu ya nishati safi ya kupikia na hivyo kuchangia kufikiwa kwa malengo ya taifa ya kuhakikisha asilimia 80 ya wananchi wanatumia nishati safi ya kupikia ifikapo 2034.










-Teknolojia, usuluhishi wa migogoro na maboresho ya sheria vipaumbele vya mafunzo

-Mawakili wakumbushwa kulinda maslahi ya Taifa, uwekezaji na usalama wa nchi

 -Mafunzo yatekeleza maelekezo ya Rais Samia ya kupitia na kuboresha sheria


Na Vero Ignatus, Michuzi TV – Arusha

Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Hamza S. Johari, leo Julai 14, 2026 amefungua rasmi mafunzo ya siku tatu kwa mawakili 650 wa Serikali yanayofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC). Mafunzo hayo yanalenga kuwaimarisha mawakili katika utekelezaji wa majukumu yao sambamba na maandalizi ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Akizungumza wakati wa ufunguzi, Mhe. Johari alisema mafunzo hayo yanalenga kuwajengea uwezo mawakili kuhusu mabadiliko yanayotokana na maendeleo ya sayansi na teknolojia, pamoja na kuhakikisha mfumo wa sheria unaendana na malengo ya Dira ya Maendeleo 2050 ili uwe kichocheo cha maendeleo ya Taifa.

Alisema mada zitakazojadiliwa zinahusisha usuluhishi wa migogoro, hususan migogoro ya kibiashara, namna ya kuweka uwiano kati ya maendeleo ya nchi na ulinzi wa wawekezaji, pamoja na kutathmini kama sheria zilizopo zinachochea mageuzi ya uchumi na maendeleo endelevu.

"Tunataka pia kuangalia jukumu la wakili katika kuimarisha uzalendo, kulinda maslahi pamoja na usalama wa Taifa. Wasipofahamu wajibu huo wanaweza kujikuta wanaingia katika matendo yanayoweza kuhatarisha usalama wa Taifa au kuathiri maslahi ya nchi kiuchumi na kijamii," alisema Mhe. Johari.

Awali, Mkurugenzi wa Uratibu na Huduma za Ushauri wa Sheria, Wakili Neema Ringo, alisema mafunzo hayo yatawawezesha mawakili kuongeza uelewa kuhusu matumizi ya teknolojia, kutambua vihatarishi vinavyotokana na maendeleo ya kidijitali, pamoja na kujadili namna ya kuboresha sheria ili ziendane na mazingira ya sasa.

Alieleza kuwa mafunzo hayo pia yanatekeleza maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, aliyemtaka Mwanasheria Mkuu wa Serikali kuratibu mapitio ya sheria zote ili kufanyiwa marekebisho, kuboreshwa au kufutwa pale zinaposhindwa kuendana na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Wakili Ringo aliongeza kuwa mafunzo hayo, yaliyoandaliwa na kuratibiwa na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, yanatoa fursa kwa mawakili kubadilishana uzoefu, kuongeza ujuzi na kujadili mabadiliko ya sheria, sayansi na teknolojia yanayoendelea duniani.

Kwa upande wake, Mwandishi Mkuu wa Sheria, Onorious Njole, alisema jumla ya mawakili 650 kutoka wizara, taasisi za Serikali, mamlaka za Serikali za Mitaa na idara mbalimbali za umma wanashiriki mafunzo hayo. Alisema lengo ni kuwajengea uwezo wa kitaaluma na kiutendaji ili waendelee kusimamia kwa ufanisi tasnia ya sheria na kuchangia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.







Skauti Mkuu wa Tanzania, Lt. Rashid Mchata, amesema ushirikiano kati ya Chama cha Skauti Tanzania (Tanzania Scouts Association-TSA) na Oryx Gas Tanzania Limited ni hatua ya kimkakati itakayowawezesha maelfu ya vijana wa Skauti na Watanzania kwa ujumla kupata maarifa, ujuzi na fursa za kushiriki katika maendeleo ya Taifa kupitia matumizi salama ya nishati safi.

Akizungumza katika hafla ya utiaji saini wa mkataba wa ushirikiano huo leo Jumatano Julai 15, 2026, Lt. Mchata amesema hafla hiyo si tukio la kawaida la kusaini hati, bali ni tamko la dhamira, daraja la fursa na mwanzo wa safari ya pamoja ya kuwaletea vijana mabadiliko chanya yatakayodumu kwa miaka mingi.

Amesema TSA inaamini kuwa kijana mwenye maarifa ni nguvu ya Taifa, mwenye ujuzi ni rasilimali muhimu ya maendeleo, huku mwenye maadili na nidhamu akiwa msingi wa mustakabali wa Tanzania.

Lt. Mchata ameeleza kuwa kupitia makubaliano hayo, Skauti Tanzania itaunganisha mtandao wake mkubwa wa vijana na utaalamu wa Oryx Gas Tanzania katika sekta ya gesi ya LPG ili kuimarisha elimu ya matumizi salama ya nishati safi, usalama wa jamii, maandalizi ya kukabiliana na dharura pamoja na kuwaongezea vijana ujuzi utakaowawezesha kujiajiri na kupata ajira.

Amesisitiza kuwa, lengo si kuwaeleza vijana kuhusu fursa zilizopo pekee, bali kuwajengea uwezo wa kuzitambua, kuzitumia na kuzalisha fursa mpya zinazochochea maendeleo ya Taifa.

Aidha, amesema TSA itasimamia utekelezaji wa ushirikiano huo kwa uwajibikaji mkubwa ili kuhakikisha unaleta matokeo yaliyokusudiwa, huku akiwataka vijana wa Skauti kutumia nafasi hiyo kujifunza, kujenga uwezo na kuwa wabunifu katika kulitumikia Taifa.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Oryx Energies Tanzania, Benoit Araman, amesema kampuni hiyo imeamua kushirikiana na Skauti baada ya kuona kuwa harakati zao zina misingi inayolingana na malengo ya Oryx ya kuitumikia jamii kupitia elimu ya matumizi salama ya gesi ya LPG.

Amesema dhima ya Skauti ya kuwa tayari wakati wote kuhudumia jamii ndiyo iliyowafanya kuitambua TSA kama mshirika sahihi wa kutekeleza programu ya utoaji elimu kuhusu matumizi salama ya gesi kwa wananchi.

Araman ameongeza kwa kusema kuwa, Oryx kwa kushirikiana na wataalamu wake itatoa mafunzo kwa wawakilishi wa Skauti kutoka maeneo mbalimbali nchini, ambao baadaye watakuwa wakufunzi na mabalozi wa kuielimisha jamii namna sahihi ya kutumia gesi ya LPG kwa usalama.

Amesema hatua hiyo itasaidia kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu matumizi salama ya nishati safi, kupunguza ajali zinazotokana na matumizi yasiyo sahihi ya gesi na kuchangia ustawi wa jamii kwa muda mrefu.

Naye Kamishna Mkuu wa Skauti Tanzania, Abubakari Mtitu, amesema, mkataba huo ni sehemu ya mkakati endelevu wa kuhakikisha vijana wanapata mafunzo ya weledi kuhusu matumizi ya nishati safi na tahadhari zinazopaswa kuzingatiwa wakati wa matumizi yake.

Ameendelea kwa kusema kuwa, ushirikiano huo unaendana na misingi ya Skauti ya kutekeleza wajibu kwa Mungu, kwa wengine na kwa nafsi binafsi, huku ukiwapa vijana nafasi ya kutumia elimu watakayopata kuwahudumia wananchi katika maeneo yao.

Mtitu amesema kupitia mafunzo hayo, vijana wa Skauti pamoja na vijana wengine wa Tanzania watawezeshwa kuwa mabalozi wa matumizi salama ya nishati safi, hatua itakayochangia kujenga jamii salama na kuifanya dunia kuwa mahali bora zaidi kuliko walivyoikuta.

Ameongeza kwa kusema kuwa, TSA itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali katika kuandaa programu zinazowajengea vijana uwezo, maadili na ujuzi unaohitajika katika kuchangia maendeleo endelevu ya Taifa.










Na Janeth Raphael - MichuziTv 

Matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini yanatarajiwa kuongezeka kwa kasi endapo wananchi wataendelea kupata taarifa sahihi, zinazoeleweka na zinazotolewa kwa ujumbe mmoja kutoka kwa wadau mbalimbali wanaohusika na sekta hiyo.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Nishati Safi ya Kupikia,  Nolasco Mlay, wakati wa ufunguzi wa Warsha ya Kuwajengea Uwezo Waandishi wa Habari na Maafisa Mawasiliano wa Serikali kutoka mikoa, wizara, taasisi na mashirika yaliyo chini ya Wizara ya Nishati kuhusu uandishi na uhamasishaji wa matumizi ya nishati safi ya kupikia. Warsha hiyo imefanyika Julai 14, 2026 mkoani Morogoro.

 Mlay amesema utoaji wa ujumbe sahihi na wenye uelewa wa pamoja ni nyenzo muhimu katika kuwasaidia wananchi kufanya maamuzi sahihi kuhusu matumizi ya teknolojia mbalimbali za nishati safi ya kupikia, ikiwemo gesi ya kupikia (LPG), umeme, biogesi, gesi asilia na mkaa mbadala.

Amesema Serikali inaendelea kutekeleza Mkakati wa Taifa wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia wenye lengo la kuhakikisha kuwa ifikapo mwaka 2034, angalau asilimia 80 ya Watanzania wanatumia nishati safi ya kupikia.

Kwa mujibu wa Mlay, baada ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kuzindua Mkakati wa Taifa wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia mwaka 2024, Serikali iliendelea kuimarisha juhudi hizo kwa kuzindua Mkakati wa Mawasiliano mwaka 2025, unaolenga kuhakikisha ujumbe unaotolewa kwa wananchi kuhusu nishati safi ya kupikia unakuwa wa pamoja, sahihi na unaoeleweka.

Ameeleza kuwa mkakati huo unalenga kuwawezesha wadau wote wanaotoa elimu kwa umma kuwa na uelewa unaofanana ili kuondoa taarifa zinazokinzana, kuongeza uhamasishaji na kuwafanya wananchi kuchagua matumizi ya nishati safi kwa manufaa ya afya zao, mazingira na maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

 Mlay amesisitiza kuwa vyombo vya habari vina nafasi ya kipekee katika kufanikisha ajenda hiyo ya kitaifa, kwani vina uwezo mkubwa wa kufikisha ujumbe kwa mamilioni ya Watanzania na kuongeza uelewa kuhusu faida za matumizi ya nishati safi ya kupikia.

Aidha, amewataka waandishi wa habari pamoja na Maafisa Mawasiliano wa Serikali kuendelea kuandika na kusambaza taarifa zenye usahihi, zinazozingatia ujumbe wa pamoja na zinazohamasisha mabadiliko ya tabia, akibainisha kuwa hatua hiyo itasaidia kupunguza upotoshaji, kuongeza uelewa wa jamii na kuharakisha utekelezaji wa malengo ya taifa ya matumizi ya nishati safi ya kupikia.



Na MWANDISHI WETU

UONGOZI mpya wa Taasisi ya Usanifu wa Kiswahili na Ushairi Tanzania (UKUTA) leo umekabidhiwa rasmi ofisi na uongozi uliopita baada ya uchaguzi mkuu uliofanyika Julai 11 mwaka huu.

Akizungumza katika hafla ya makabidhiano hayo yaliyofanyika katika ukumbi wa Anatouglou, jijini Dar es Salaam, yalipo makao makuu ya UKUTA, Mwenyekiti wa taasisi hiyo taifa, Hussein Ally Jimbika, amesema , wamejipanga kusimamia kikamilifu usanifu wa lugha ya Kiswahili na ushairi nchini.

Amesema, UKUTA itaendelea kuenzi jitihada za kubwa za viongozi na waasisi wa taasisi hiyo hususan Baba wa Taifa hayati Mwalimu Julius Nyerere, ambaye ndiyo mtu wa kwanza kuunda chombo hiki kabla ya uhuru kwa kushirikiana na hayati Abeid Aman Karume na Sheikh Amri Abeid Karuta.

Ameeleza UKUTA ilitoa mchango mkubwa katika kufanikisha taifa kupata uhuru na kwamba uongozi wa taasisi hiyo utaendelea kufuata nyendo zao kuhakikisha safari ya kuenzi Kiswahili inafanikiwa.

“Wazee hawa walikuwa na makusudio makubwa ya Kiswahili kuwa ni nyenzo muhimu ya kupata uhuru na ustawi wa taifa.

Hivyo Uongozi mpya tutashirikiana na wenzetu kuhakikisha lengo la waasisi hawa linaendelewa na kufikiwa katika kukuza Kiswahili,”amesema Jimbika.

Jimbika alisema lengo lingine ni kuongeza usajili wa wanachama kwani mpaka sasa UKUTA inawachama 2050 tu.

Katibu Mkuu wa UKUTA, Abubakyr Kiaibamba, amewarika wanachama wa katika ofisi za makao makuu ya taasisi hiyo zilizopo katika jengo la Anatouglou kwa uratibu wa shughuli zote za taasisi na kujisajili .

“Malengo yangu ni kuhakikisha tunakifanya Kiswahili kuwa bidhaa. Hii ndiyo kazi anayoifanya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan. Tutahakikisha vitabu vinaandikwa, mashairi yanatungwa na tunawakomboa washairi kuchumi kupitia kazi zao,”amesema Kiaibamba.

Akikabidhi nyaraka za ofisi Katibu Mkuu mstaafu Hassan Ligile, ameupongeza uongozi huo mpya kushinda katika uchaguzi wa kidermokrasia uliofanyika na kwamba wataendelea kutoa ushirikiano kuhakikisha UKUTA inasonga mbele huku akijivunia mafanikio yaliyopatikana chini ya uongozi wake.









Jane Mwakyoma, July 15, 2026, Rukwa.

MKUU wa Mkoa wa Rukwa Charles Makongoro Nyerere ameipongeza Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi kwa kufanikiwa kupata hati safi akieleza kuwa mafanikio hayo ni kielelezo cha usimamizi bora wa fedha za umma na uwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu ya Serikali.

Nyerere ametoa pongezi wakati akizungumza katika Baraza Maalum la Madiwani la kujadili Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG).

Amesema mafanikio hayo yametokana na ufungaji mzuri wa vitabu vya hesabu za Serikali, uzingatiaji wa sheria, kanuni na taratibu za matumizi ya fedha za umma, usimamizi madhubuti wa rasilimali, ukusanyaji mzuri wa mapato, utekelezaji wa bajeti kwa ufanisi, pamoja na ushirikiano imara kati ya Menejimenti ya Halmashauri na wadau mbalimbali wa maendeleo.

Aidha amesisitiza kuwa mafanikio hayo yanaendelea kuimarisha uwajibikaji, uwazi na usimamizi bora wa rasilimali za umma kwa manufaa ya wananchi wa Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi.

Pia ameitaka Halmashauri kuendeleza juhudi hizo ili kudumisha viwango vya utendaji na utoaji bora wa huduma kwa wananchi.









Top News