Farida Mangube, Morogoro

Wataalamu wameonya kuwa kuongezeka kwa matumizi ya kemikali za kilimo bila kuzingatia kanuni za kitaalamu kunaweza kuongeza hatari ya magonjwa, kuathiri ubora wa mazao na kuhatarisha mazingira, wakitaka wakulima kuelekea zaidi katika matumizi ya mbinu za kilimo ikolojia.

Akizungumza katika mkutano ulioandaliwa na Sekretarieti ya Kitovu cha Kilimo Ikolojia kupitia Mradi wa Mtandao wa Utafiti wa Ikolojia Kusini mwa Afrika (RAENS) mkoani Morogoro, Profesa Kalunde Sibuga wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) alisema matumizi yasiyo sahihi ya kemikali yanaweza kuathiri afya za wakulima, walaji na mazingira, huku mabaki ya kemikali kwenye mazao yakihatarisha usalama wa chakula.

Alisema kilimo ikolojia ni suluhisho linaloweza kuongeza uzalishaji wa mazao kwa kutumia mbinu rafiki kwa mazingira kama mbolea za asili, udhibiti wa wadudu kwa njia za kibaiolojia na usimamizi endelevu wa ardhi na maji, akisisitiza umuhimu wa kutoa elimu kwa wakulima kuhusu matumizi salama ya pembejeo.

Kwa upande wake, Mratibu wa RAENS, Profesa Dismas Mwaseba, alisema pamoja na uwepo wa sera zinazounga mkono kilimo endelevu, bado sekta hiyo inakabiliwa na changamoto zikiwemo ukosefu wa masoko ya uhakika, uelewa mdogo wa wakulima na upungufu wa huduma za mafunzo na ugani kuhusu kilimo ikolojia.

Naye mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Bw. Gosbert Chobya, alisema Serikali inaendelea kutambua mchango wa kilimo ikolojia katika kuongeza tija, kulinda mazingira na kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, huku akisisitiza ushirikiano wa wadau mbalimbali katika kuboresha sera na mazingira ya utekelezaji wa kilimo hicho nchini.






Na ABDU MADENGE, WAF - DODOMA

Baraza la Tiba Asili na Tiba Mbadala nchini limefuta usajili wa dawa ya Powaful Banana Medicine, kupiga marufuku uingizwaji na matumizi ya dawa ya Vitamax, pamoja na kuamuru kuondolewa sokoni kwa toleo namba MN1060 la dawa ya Joy.

Hatua hiyo imechukuliwa baada ya ukaguzi na vipimo vya maabara kubaini uwepo wa mchanganyiko wa kemikali hatari za kisasa na sumu kuvu kwenye bidhaa hizo kinyume cha sheria.

Hayo yamebainishwa na Mwenyekiti wa Baraza hilo, Prof. Nicolao Joseph Otieno, wakati wa mkutano na waandishi wa habari uliofanyika katika Ofisi za Wizara ya Afya Juni 05, 2026 Mkoani Dodoma ambapo ameeleza maamuzi hayo yanajiri kufuatia zoezi maalum la ufuatiliaji wa dawa sokoni (Post Market Surveillance) lililofanyika katika mwaka wa fedha wa 2025/2026, ambalo lilibaini ukiukwaji mkubwa wa Kanuni za Usimamizi wa Dawa za Tiba Asili kifungu cha 13(1)(a) na (b).

Prof. Otieno ameongeza kuwa Uchunguzi wa kimaabara umeonesha dawa ya Powaful Banana (inayotengenezwa na Powaful Products Company Ltd) na Vitamax (kutoka kampuni ya Superfood International ya Malaysia), ambazo zimekuwa zikitumika kuongeza nguvu za kiume, zimechakachuliwa kwa kuongezewa kemikali za kisasa za Sildenafil, Tadalafil, pamoja na dawa za maumivu aina ya Tramadol na Paracetamol.

“Tunaonya matumizi ya kemikali hizo bila usimamizi wa daktari yanaweza kusababisha magonjwa ya moyo, kufeli kwa ini na figo, shinikizo la damu, na hata vifo vya ghafla.” amesema Prof . Otieno.

Sambamba na hatua hizo, Baraza pia limebaini kuwa toleo namba MN1060 la dawa ya Joy (Usajili Na. TZ25TM0010) lina kiwango kikubwa cha sumu kuvu (mycotoxins) kinachoweza kusababisha saratani ya ini na uharibifu wa figo. Hali hii imetajwa kutokana na kutokuzingatiwa kwa viwango bora vya ukaushaji na uhifadhi wakati wa uzalishaji.

“Baraza tunatoa onyo kali kwa watengenezaji wote nchini ambao dawa zao zimebainika kuwa na mapungufu katika vifungashio, taarifa za lebo, ujazo, na maelezo ya dozi, tunawataka kufanya maboresho ya haraka kulingana na vigezo vya usajili kwa lengo la kulinda afya na usalama wa watumiaji.” amesema na kuongeza Prof. Otieno.





 

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, , amewataka wanafunzi wa sheria nchini kujenga taaluma zao katika misingi ya nidhamu, ubunifu na uzalendo ili waweze kushindana katika soko la ajira la kimataifa linalozidi kuwa na ushindani.

Ridhiwani alitoa wito huo Juni 5, 2026, alipokuwa akizungumza katika maadhimisho ya Siku ya Kazi na Taaluma ya Shule ya Sheria ya yaliyofanyika jijini Dar es Salaam.

Alisema mafanikio katika taaluma za kisasa hayawezi kupatikana bila wataalamu kuzingatia maadili, hususan nidhamu, uzalendo na umahiri wa kitaaluma, mambo ambayo ni muhimu katika kujenga uwezo wa kushindana ndani na nje ya mipaka ya nchi.

“Ni muhimu kwa wanafunzi wa sheria kutambua kuwa dunia ya sasa inahitaji wataalamu wenye uwezo wa kushindana kimataifa huku wakizingatia maadili ya taaluma zao na kulinda maslahi ya taifa lao,” alisema.

Aidha, Ridhiwani alisema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia imeendelea kufanya mageuzi makubwa katika sekta ya sheria na haki kwa lengo la kuimarisha utoaji wa huduma za haki nchini.

Alitaja baadhi ya hatua zilizochukuliwa kuwa ni pamoja na matumizi ya teknolojia katika mfumo wa haki, uwekezaji katika miundombinu ya utoaji haki pamoja na kuhamasisha matumizi ya mifumo mbadala ya utatuzi wa migogoro.

Kwa mujibu wa Ridhiwani, mageuzi hayo yanalenga kuwawezesha wanasheria na watendaji wa vyombo vya haki jinai kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi huku yakichangia kujenga mazingira bora ya maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

Alisisitiza kuwa wataalamu wa sheria wana nafasi muhimu katika kulinda maslahi ya taifa, kuimarisha utawala wa sheria na kuchochea maendeleo endelevu kupitia usimamizi wa haki na sheria.

Maadhimisho hayo yalikusanya wanafunzi, wahadhiri na wadau mbalimbali wa sekta ya sheria kujadili fursa na changamoto zinazokabili taaluma hiyo katika mazingira ya dunia yanayobadilika kwa kasi.
Na Beda Msimbe, TBN, aliyekuwa Urusi

IJUMAA, Juni 5, 2026, ilikuwa siku ya kihistoria na ya kipekee wakati Rais wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, alipokuwa akizungumza mbele ya viongozi wa dunia katika Jukwaa la Kimataifa la Uchumi la St. Petersburg (St. Petersburg International Economic Forum) na kuwasilisha hoja nzito zenye mashiko, akibeba sauti ya Watanzania wote huku akiweka wazi fursa zinazopatikana Tanzania pamoja na mwelekeo mpya wa nchi katika kujenga uchumi wa kisasa.

Jukwaa hilo lilikuwa sehemu muhimu ya ziara ya Rais Samia ambayo haikuwa tu ya kiitifaki, bali pia ya kufungua milango ya fursa za kiuchumi na kijamii.

Jinsi Rais Samia alivyopokewa na kukirimiwa nchini Urusi katika shughuli zote zilizomhusu, ilionesha taswira ya urafiki wa dhati na uelewano mkubwa kati yake na mwenyeji wake, Rais Vladimir Putin. Ziara hiyo ilifufua historia ya ushirikiano wa mataifa hayo mawili na kuweka wazi haja ya sasa ya kusaidiana katika kuleta ukombozi wa kiuchumi na ustawi wa jamii baada ya ukombozi wa kisiasa.

Akiwa katika jukwaa hilo la kiuchumi, hotuba ya Rais Samia iliwafanya washiriki wengi kutafakari kwa kina kutokana na hoja zake zilizojikita katika uchambuzi wa masuala ya dunia na umuhimu wa mabadiliko ya kimfumo katika uchumi wa kimataifa.

Rais Samia alitoa hoja yenye kuchokoza fikra aliposema kuwa ifikapo mwaka 2050, mtu mmoja kati ya wanne duniani atakuwa Mwafrika. Takwimu hiyo iliambatana na swali lenye uzito mkubwa: “Je, Afrika itastawi na kukua kwa masharti ya nani, na kwa modeli ipi ya uchumi?”

Swali hilo lilikuwa na mantiki kubwa katika kipindi ambacho siasa za kijiografia zimeendelea kuyumbisha ushirikiano wa kawaida wa kimataifa na kujaza mazingira ya masharti, ushindani na udhibiti wa kiuchumi unaozikandamiza nchi maskini.

Katika msingi huo wa kimantiki, Rais Samia alikuwa akiitaka dunia isiisitiri Afrika wala kuipangia mustakabali wake, bali itambue ukweli na kuiacha Afrika ijiamulie mambo yake yenyewe.

Mathalani, Afrika kwa sasa ina Ajenda 2063 pamoja na soko la pamoja la AfCFTA, lakini bado kuna mataifa yanayoendelea kuingilia masuala ya bara hilo na kuwagawa Waafrika ili waendelee kuonekana wanahitaji msaada wa kudumu katika kutatua changamoto zinazowakabili.

Rais Vladimir Putin aliunga mkono hoja hiyo, jambo lililoibua miguno ya ridhaa na vigelegele ukumbini. Kwa hakika, yapo mambo mengi ambayo Waafrika wanaweza kuyafanya wenyewe kwa manufaa yao na ya dunia kwa ujumla.

Mambo yaliyoguswa

Katika hotuba yake na ziara hiyo ya Urusi, Rais Samia aligusa masuala mengi muhimu. Hapa tunaweza kuangazia maeneo makubwa yaliyobebwa na ziara hiyo pamoja na namna makubaliano mbalimbali yalivyohitimishwa kwa mafanikio makubwa kwa Tanzania.

Ikumbukwe kuwa ziara ya Rais Samia, ambayo pia aliambatana na wafanyabiashara wa Tanzania, imeikumbusha dunia kuhusu mizizi imara ya kidiplomasia kati ya Tanzania na Urusi. Mahusiano hayo yana historia ndefu tangu miaka ya mwanzo ya uhuru, ambapo siku mbili tu baada ya Tanganyika kupata uhuru, Urusi ilituma salamu za pongezi; hali iliyojirudia pia wakati wa Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar.

Mbele ya wawekezaji, Rais Samia alibainisha kuwa uchumi wa Tanzania unakua kwa kasi ya takribani asilimia sita, hali inayoiweka nchi miongoni mwa uchumi unaokua kwa kasi zaidi barani Afrika.

Aidha, alitangaza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayolenga kumfikisha kila Mtanzania kwenye kipato cha wastani cha dola za Marekani 7,000 huku akielezea kwa kina fursa mbalimbali za uwekezaji na biashara zilizopo nchini Tanzania.

Hotuba hiyo iliyopigiwa makofi mara kwa mara iliwavutia wawekezaji wengi wa Kirusi, ambapo sekta binafsi ya Urusi ilikiri kuwa Tanzania ni soko salama lenye utulivu wa kisiasa unaowezesha ukuaji wa mitaji na biashara.

Mbali na hayo, Rais Samia alieleza kuhusu mapinduzi makubwa ya miundombinu yanayoendelea nchini, hususan katika sekta ya reli na bandari. Katika mikutano ya pamoja na wafanyabiashara wa Tanzania na Urusi, alifafanua kwa kina kuhusu ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR) inayounganisha Bandari ya Dar es Salaam na nchi za Rwanda, Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), pamoja na manufaa yake kwa ukanda mzima wa Afrika Mashariki na Kati.

Pia alieleza mpango wa miaka mitano wa kuipanua reli hiyo kuanzia mwaka 2026 hadi 2031 kuelekea Musoma na kuunganisha ukanda wa kusini kupitia Malawi hadi Msumbiji. Urusi, ikiwa na uzoefu mkubwa katika teknolojia ya reli na usafirishaji, ilionesha nia ya kutoa utaalamu wa kihandisi pamoja na mitambo ya kusaidia kuharakisha ujenzi wa reli hizo za kikanda.

Suala la maboresho ya mazingira ya uwekezaji na mfumo wa usajili wa saa 24 lilizua msisimko mkubwa miongoni mwa washiriki. Rais Samia alieleza kuwa uwekezaji umeongezeka kutoka dola bilioni tatu mwaka 2021 hadi dola bilioni 12 mwaka 2025 kutokana na maboresho ya mifumo ya uwekezaji, ikiwemo usajili wa kampuni unaokamilika ndani ya saa 24.

Kutokana na mafanikio hayo, Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) pamoja na taasisi za uwekezaji za Urusi zilisaini mikataba ya ushirikiano. Hatua hiyo ilipokelewa kwa furaha kubwa, ikionesha namna Tanzania ilivyojidhatiti kupunguza urasimu katika uwekezaji.

Aidha, miradi ya Eneo Maalum la Kiuchumi la Bagamoyo pamoja na Bandari ya Kimataifa ya Mizigo ya Mangapwani Zanzibar ilipewa kipaumbele na makampuni makubwa ya Urusi yanayojihusisha na usafirishaji wa baharini. Makampuni hayo yalikubali kutuma timu za wataalamu nchini Tanzania kufanya upembuzi yakinifu wa namna ya kuwekeza katika miradi hiyo.

Katika sekta ya madini, Rais Samia alisisitiza umuhimu wa kuongeza thamani ya madini ndani ya nchi. Tanzania ina utajiri mkubwa wa dhahabu, uranium, nickel, graphite, helium pamoja na madini adimu.

“Hatutaki tena kuuza malighafi pekee; tunataka viwanda vya usindikaji hapa nchini,” alisema Rais Samia.

Urusi, ambayo ni miongoni mwa mataifa yenye nguvu katika sekta ya madini, ilionesha utayari wa kushirikiana na Tanzania katika kujenga viwanda vya uchakataji na kuongeza thamani ya madini kabla ya kusafirishwa kwenda nje ya nchi.

Katika ziara hiyo, Rais Samia alidhihirisha wazi namna Tanzania ilivyo tayari kwa biashara, ubunifu na ushirikiano wa kimataifa unaolenga kukuza uchumi na ustawi wa wananchi wake.

Wakati Rais Samia akihitimisha hotuba yake katika jukwaa la St. Petersburg kwa kutoa shukrani za dhati kwa Rais Vladimir Putin kwa ukarimu wake, viongozi hao wawili walionesha tabasamu la furaha, ishara iliyotafsiriwa kama mwanzo mpya wa ushirikiano wa dhahabu kati ya Tanzania na Urusi.

Na Mwandishi Wetu

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Ridhiwani Kikwete, amewataka wanafunzi wa sheria nchini kujenga taaluma zao katika misingi ya nidhamu, ubunifu na uzalendo ili waweze kushindana katika soko la ajira la kimataifa linalozidi kuwa na ushindani mkubwa.

Ridhiwani alitoa wito, wakati akizungumza katika hafla ya Siku ya Kazi na Taaluma ya Shule ya Sheria ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam iliyofanyika jijini Dar es Salaam.

Alisema mafanikio ya taaluma katika dunia ya sasa hayawezi kupatikana bila wataalamu kuwa na uwezo wa kushindana nje ya mipaka ya nchi zao huku wakizingatia maadili ya kazi, hususan nidhamu, uzalendo na umahiri katika fani zao.

“Ni muhimu kwa wanafunzi wa sheria kuelewa kuwa taaluma zao zinahitaji siyo tu maarifa ya kisheria, bali pia maadili, nidhamu na uzalendo vitakavyowasaidia kuwa wataalamu wenye ushindani na mchango chanya kwa taifa,” alisema.

Aidha, Ridhiwani aliwaeleza wanafunzi hao kuhusu hatua zilizochukuliwa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Samia Suluhu Hassan katika kuimarisha sekta ya sheria na utoaji wa haki nchini.

Alisema serikali imeendelea kufanya mageuzi mbalimbali ikiwemo kuboresha mfumo wa haki, kuongeza matumizi ya teknolojia katika utoaji wa huduma za kisheria, kuwekeza katika miundombinu ya utoaji haki na kuhamasisha matumizi ya mifumo mbadala ya utatuzi wa migogoro.

Kwa mujibu wa Ridhiwani, maboresho hayo yanalenga kuwawezesha wanasheria na wasimamizi wa vyombo vya haki jinai kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi, sambamba na kujenga mazingira bora ya utoaji haki nchini.

Alisisitiza kuwa sekta imara ya sheria na haki ni nguzo muhimu katika kuharakisha maendeleo ya kiuchumi na kijamii, huku wataalamu wa sheria wakibeba jukumu kubwa la kulinda maslahi ya taifa na kuimarisha utawala bora.






BODI ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA) imeshiriki katika Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Jukwaa la Wasimamizi wa Taaluma ya Ukaguzi Afrika (African Forum of Independent Accounting and Auditing Regulators (AFIAAR) wa mwaka 2026, unaofanyika mjini Port Louis, Mauritius kuanzia tarehe 2 hadi 5 Juni 2026.

Katika Mkutano huo, Mkurugenzi Mtendaji wa NBAA, CPA Prof. Siasa Mzenzi, alichaguliwa kuwa Makamu Mwenyekiti wa AFIAAR. Pamoja na Mkurugenzi Mtendaji, NBAA imewakilishwa na CPA Pius Maneno, Mkurugenzi Mtendaji Mstaafu wa NBAA na Makamu Mwenyekiti anayemaliza muda wake wa jukwaa hilo; CPA Winnington Makaka, Mkuu wa Sehemu ya Ubora wa Ukaguzi (AQR); pamoja na Magreth Kageya, Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na Mawasiliano cha NBAA.

Lengo la mkutano huo ni kuwakutanisha wasimamizi wa taaluma ya Uhasibu na Ukaguzi barani Afrika ili kujadili masuala mbalimbali yanayohusu taaluma hiyo, hususan hali ya ubora wa ukaguzi. Majadiliano hayo yanalenga kuimarisha ubora wa taarifa za ukaguzi wa makampuni, jambo litakalosaidia kukuza uchumi wa Afrika kwa kuongeza imani ya wawekezaji kupitia taarifa sahihi na za kuaminika za kifedha.

Akizungumza katika mkutano huo, Mkurugenzi Mtendaji wa NBAA na Makamu Mwenyekiti wa AFIAAR, CPA Prof. Siasa Mzenzi, alisema: “Mkutano huu ni muhimu kwa taasisi yetu na Tanzania kwa ujumla, kwani umetupatia fursa ya kujifunza na kubadilishana uzoefu kuhusu mbinu bora za usimamizi wa taaluma ya ukaguzi. Maarifa haya yatasaidia kuboresha ubora wa huduma za ukaguzi nchini na hivyo kuongeza uaminifu wa taarifa za kifedha zinazotolewa na taasisi na makampuni mbalimbali.”

Mkutano wa AFIAAR unawakutanisha wadau mbalimbali wa usimamizi wa taaluma ya ukaguzi kutoka nchi mbalimbali za Afrika kwa lengo la kuimarisha ushirikiano, kubadilishana uzoefu na kujadili mikakati ya kuendeleza ubora wa ukaguzi barani humo.











Pamela Mollel, Arusha

Kampuni ya House of Canvas Ltd imewataka wadau mbalimbali kujitokeza kwa wingi kutembelea banda lake katika Maonesho ya Karibu-Kilifair 2026 na kujionea bidhaa zake zenye ubora wa hali ya juu, uimara na uwezo wa kudumu kwa muda mrefu

Akizungumza na waandishi wa habari katika maonesho hayo yanayoendelea mkoani Arusha, Mkurugenzi wa kampuni hiyo, Evans Ogiloh, amesema kuwa mwaka huu wamekuja na bidhaa mpya nyingi za kisasa zilizoboreshwa ili kukidhi mahitaji ya wateja wa ndani na nje ya nchi

Amesema House of Canvas Ltd imejijengea sifa ya kuzalisha bidhaa bora na zinazodumu kwa muda mrefu, jambo ambalo limeifanya kampuni hiyo kuendelea kuaminika na wateja wake katika sekta mbalimbali

"Mwaka huu tumekuja na bidhaa mpya nyingi zenye ubora wa hali ya juu na zinazodumu kwa muda mrefu

Tunawaalika wadau wote kutembelea banda letu ili wajionee ubunifu na ubora wa bidhaa tunazozalisha," amesema Ogiloh

Aidha, amewapongeza waandaaji wa Maonesho ya Karibu-Kilifair 2026 kwa maandalizi mazuri yaliyofanyika mwaka huu, akibainisha kuwa yameboreshwa kwa kiwango kikubwa ikilinganishwa na mwaka uliopita

"Kwa kweli nimefurahishwa sana na maandalizi ya maonesho ya mwaka huu. Waandaaji wamejipanga vizuri na mazingira ya maonesho ni bora zaidi kuliko mwaka jana," ameongeza

Ogiloh amesema kampuni hiyo inajishughulisha na utengenezaji wa mahema mbalimbali ikiwemo mahema ya kambi za milimani, mahema ya utalii pamoja na bidhaa nyingine za canvas zinazotumika katika shughuli mbalimbali.

Amesisitiza kuwa House of Canvas Ltd itaendelea kubuni na kuzalisha bidhaa zenye viwango vya juu vya ubora ili kukidhi mahitaji ya soko na kuchangia maendeleo ya sekta ya utalii na biashara nchini.






Mkurugenzi wa Kadama English Medium Primary School, Leticia Pastory, ameibuka mshindi wa Tuzo ya Mmiliki Bora wa Shule wa Kike Mkoa wa Geita kwa mwaka 2026. Tuzo hiyo imetolewa kwa kutambua mchango wake mkubwa kwenye sekta ya elimu.

Tuzo ilikabidhiwa rasmi Juni 6, 2026 na Mwenyekiti wa UWT Taifa na Mbunge, Mary Chatanda, kwenye Tamasha la Mwanamke wa Dhahabu 2026 lililofanyika Golden Social Hall, Geita. Tukio hilo liliandaliwa na Geita Women and Youth Foundation inayoongozwa na Mkurugenzi Cecylia Miraji.

Hafla hiyo muhimu ilihudhuriwa na Mkuu wa Mkoa Martine Shigela, Mbunge wa Geita Mjini Chacha Wambura, na Mkurugenzi wa Manispaa Yefred Myenzi.

Baada ya kupokea tuzo, Leticia alisema mafanikio hayo yanatokana na jitihada za miaka mingi za kuinua elimu Geita. Alibainisha kuwa Kadama imejijengea heshima kitaifa kutokana na matokeo mazuri na mazingira bora ya masomo.

Alikumbusha kuwa mwaka 2018 shule hiyo iliweka historia baada ya mwanafunzi wake kushika nafasi ya kwanza kitaifa na mwingine wa pili kwenye matokeo ya darasa la saba.

"Ni faraja kubwa. Tuzo hii inatupa nguvu kuendelea kutoa elimu bora na kuhamasisha wanawake wenzangu watumie nafasi zao kuleta mabadiliko," alisema Leticia.









Zaidi ya wanaushirika 2,000 wamepata mafunzo ya ushirika na maendeleo binafsi kupitia Jukwaa la Tano la Maendeleo ya Ushirika Mkoa wa Dodoma lililofanyika Juni 5 hadi 6, 2026 jijini Dodoma, likiwa na lengo la kuwakutanisha wadau wa ushirika kujadili mafanikio, changamoto na fursa za maendeleo katika sekta hiyo.

Akizungumza wakati wa kuwasilisha taarifa ya maendeleo ya ushirika mbele ya mgeni rasmi, Naibu Waziri wa Kilimo, Mhe. David Silinde, Mrajisi Msaidizi wa Vyama vya Ushirika Mkoa wa Dodoma, Joseph Chintika, Juni 6, 2026.

Amesema ushirika utaendelea kuwa na tija iwapo wanachama watazingatia uadilifu, utoaji wa huduma bila ubaguzi pamoja na kuhakikisha mazao yanayouzwa yanakuwa safi na yenye ubora, ikiwa ni moja ya nyenzo muhimu katika kuwasaidia wakulima kupata bei nzuri na kuongeza ushindani wa bidhaa zao katika soko.

Katika hatua nyingine, Chintika amesema matumizi ya mifumo ya kidijitali katika vyama vya ushirika mkoani Dodoma yameongezeka kutoka vyama 40 hadi 60, sawa na ongezeko la asilimia 23, hatua ambayo imechangiwa na juhudi za kuhamasisha matumizi ya teknolojia katika usimamizi wa shughuli za ushirika.

Aidha, amesema usajili wa wanachama umeongezeka kwa asilimia nne kutokana na mwamko unaoendelea kutolewa kwa wananchi kuhusu umuhimu wa kujiunga na vyama vya ushirika.

Ametoa shukrani kwa Mrajisi Mkuu wa Vyama vya Ushirika nchini kwa mchango wake katika kuimarisha na kukuza sekta ya ushirika nchini, hali ambayo imewezesha vyama vingi kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma kwa wanachama.

Kwa mujibu wa Chintika, Mkoa wa Dodoma una jumla ya vyama vya ushirika 127 vinavyojumuisha SACCOS, vyama vya mazao na vyama vingine vya ushirika, vyenye jumla ya wanachama 22,228.

Amesema hadi sasa vyama 82 kati ya hivyo vimefikiwa na kupewa elimu mbalimbali za ushirika kwa lengo la kuongeza ufanisi, uwajibikaji na tija katika shughuli zao za kila siku.




Serikali imeziagiza Mamlaka ya Udhibiti wa Nafaka na Mazao Mchanganyiko (COPRA) na Soko la Bidhaa Tanzania (TMX) kuhakikisha mazao ya kimkakati yanayozalishwa na wanaushirika yanakusanywa na kuuzwa kupitia mfumo wa stakabadhi ghalani kwa vyama vya ushirika pekee, badala ya wanunuzi binafsi.

Maagizo hayo yametolewa na Naibu Waziri wa Kilimo, Mhe. David Silinde, wakati akifunga Jukwaa la Tano la Maendeleo ya Ushirika Mkoa wa Dodoma Juni 6, 2026.

Mhe. Silinde amesema mfumo wa ushirika umeendelea kuthibitika kuwanufaisha zaidi wakulima, hivyo ni muhimu kuhakikisha mazao ya kimkakati yanauzwa kupitia vyama vya ushirika ili kuongeza tija na manufaa kwa wazalishaji.

Aidha, amezitaka COPRA na TMX kutafuta njia mbadala za kuboresha bei za mazao kufuatia malalamiko ya wakulima kuhusu bei za kuanzia kwenye minada kuwa ndogo na kutokidhi matarajio yao, amesema taasisi hizo zinapaswa kuhakikisha wakulima wanapata bei nzuri na zenye kuridhisha ili kunufaika ipasavyo na uzalishaji wao.

Naibu Waziri huyo amesema Serikali itaendelea kuboresha mazingira ya kisera na kisheria kwa lengo la kuimarisha sekta ya ushirika nchini, huku ikihakikisha wakulima wanazalisha mazao yenye ubora wa ushindani katika soko la ndani na la kimataifa.

Katika kuongeza upatikanaji wa mitaji, amezitaka benki hususan Benki ya Ushirika kutoa mikopo yenye riba nafuu kwa vyama vya ushirika na wanaushirika binafsi ili kuongeza uzalishaji na tija katika sekta ya kilimo.

Sambamba na hilo, ameitaka Shirika la Ukaguzi na Usimamizi wa Vyama vya Ushirika (COASCO) kuhakikisha vyama vyote vya ushirika vinakaguliwa kwa wakati, huku akiitaka Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania (TCDC) kuongeza kasi ya usimamizi na ufuatiliaji wa vyama vya ushirika nchini.

Mhe. Silinde amesema ushirika ni nyenzo muhimu katika kukuza uchumi wa taifa, kuongeza ajira za kudumu na za muda mfupi pamoja na kuboresha maisha ya wananchi.

Aidha, ametoa onyo kwa baadhi ya wanaushirika wenye tabia ya kujinufaisha binafsi kwa gharama ya wanachama wengine kuacha mara moja vitendo hivyo, akieleza kuwa vinaweza kusababisha migogoro, chuki, wizi na kupoteza malengo ya msingi ya ushirika.

Amesisitiza kuwa ushirika una mchango mkubwa katika kuunganisha nguvu za pamoja, kulinda wakulima dhidi ya unyonyaji, kuchochea ubunifu na kuimarisha mafunzo ya pamoja kwa wanachama, jambo linalochangia maendeleo ya kijamii na kiuchumi nchini.


WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali imejipanga kuanza ujenzi wa barabara ya Mafinga–Mgololo kwa kiwango cha lami katika mwaka wa fedha 2026/2027 huku ikiendelea kutekeleza miradi ya kuimarisha miundombinu ya umeme ili kuondoa changamoto ya kukatika kwa umeme katika Wilaya ya Mufindi.

Amesema hayo jana Jumamosi (Juni 6, 2026) alipokuwa akizungumza na kusikiliza kero za wananchi wa Halmashauri ya Mji wa Mafinga mkoani Iringa.

Dkt. Mwigulu alisema barabara ya Mafinga–Mgololo ni miongoni mwa miradi ambayo utekelezaji wake ulipungua kasi kutokana na Serikali kuelekeza nguvu katika kukamilisha miradi mikubwa ya kimkakati ikiwemo Mradi wa Kuzalisha Umeme wa Julius Nyerere (JNHPP), Reli ya Kisasa (SGR) na Daraja la Kigongo–Busisi.

“Nilikuwepo pale pale kwenye chungu, najua kona kona zile, najua ule ukoko utatoka wapi, fedha zije na barabara hii ianze kujengwa. Nitaisimamia na nitaifuatilia kwa sababu inaungana na ahadi za Mheshimiwa Rais na ahadi za Serikali kwa wananchi,” alisema.

Alisema Serikali imeanza utekelezaji wa mpango wa kufufua miradi ambayo mikataba yake ilishasainiwa pamoja na ile ambayo wakandarasi walikuwa bado hawajapewa malipo ya awali ili waweze kuingia maeneo ya kazi.

Kuhusu huduma ya maji, Dkt. Mwigulu alisema Serikali itaendelea kusimamia utekelezaji wa mradi wa maji wa miji 28 ambao unalenga kuongeza upatikanaji wa maji katika Mji wa Mafinga na maeneo ya jirani. Alisema mradi huo ni miongoni mwa miradi ambayo awali ilikumbwa na changamoto za upatikanaji wa fedha baada ya kusainiwa kabla ya fedha kupatikana, lakini sasa Serikali imeweka utaratibu wa kuhakikisha fedha za miradi ya maji zinapelekwa moja kwa moja kwenye mifuko ya maji ili kuharakisha utekelezaji wake.

“Maji ni jambo la lazima, maji ni maisha. Mradi huu ni miongoni mwa miradi nitakayofuatilia kwa karibu ili ukamilike na wananchi wa Mafinga wapate huduma ya maji ya uhakika,” alisema.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Nishati, Salome Makamba alisema Serikali imetenga shilingi bilioni 3.9 kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya umeme katika Wilaya ya Mufindi ikiwemo kutenganisha laini zinazohudumia viwanda na zile zinazohudumia matumizi ya majumbani.

Alisema Serikali pia inaendelea na ujenzi wa kituo cha kupoza umeme katika eneo la Kisada pamoja na kuimarisha mtandao wa usambazaji wa umeme ili kuongeza upatikanaji wa umeme wa uhakika kwa wananchi na viwanda vya Mafinga.

Naye Naibu Waziri wa Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI), Dkt. Jafar Seif alisema Serikali kupitia Mradi wa TACTIC inaendelea kuboresha miundombinu ya Halmashauri ya Mji wa Mafinga ikiwemo ujenzi wa barabara za lami zenye urefu wa kilomita 11.8 pamoja na miundombinu ya soko la kisasa na stendi ya mabasi kwa lengo la kuboresha huduma za usafiri, biashara na kuchochea ukuaji wa uchumi wa mji huo.

Alisema miradi hiyo itatekelezwa kupitia awamu ya tatu ya Mradi wa TACTIC na itanufaisha wananchi wa Mafinga kwa kuboresha mazingira ya biashara, usafiri na utoaji wa huduma za kijamii.

Dkt. Seif pia alisema Serikali imeendelea kuimarisha huduma za afya katika Mji wa Mafinga ikiwemo kukamilisha mtambo wa kuzalisha hewa tiba (Oxygen Plant) ambao utahudumia Mkoa wa Iringa na maeneo mengine ya Nyanda za Juu Kusini. Alisema uwekezaji huo ni sehemu ya juhudi za Serikali za kuimarisha huduma za matibabu ya dharura na kuhakikisha upatikanaji wa hewa tiba katika hospitali za umma.

Awali, Mbunge wa Mafinga Mjini, Dickson Lutevele aliiomba Serikali kuharakisha utekelezaji wa mradi wa barabara ya Mafinga–Mgololo, kukamilisha mradi wa maji wa miji 28, kuimarisha huduma ya umeme pamoja na kuharakisha utekelezaji wa miradi ya TACTIC kutokana na umuhimu wake katika kukuza shughuli za kiuchumi, viwanda na ustawi wa wananchi.





Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) kinatarajia kuadhimisha Maadhimisho ya 11 ya Wiki ya Utafiti na Ubunifu kuanzia Juni 9 hadi 11, 2026, katika Kampasi ya Mwalimu Julius Nyerere, huku Waziri wa Madini, Anthony Mavunde, akitarajiwa kuwa mgeni rasmi.

Maadhimisho hayo yatakayowakutanisha watafiti, wabunifu, wanafunzi, sekta binafsi, taasisi za umma na wadau wa maendeleo, yanalenga kuonesha mchango wa utafiti na ubunifu katika kuharakisha maendeleo ya taifa na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Kaimu Naibu Makamu Mkuu wa Chuo anayeshughulikia Utafiti, Profesa Nelson Boniface, alisema maadhimisho ya mwaka huu yataongozwa na kaulimbiu isemayo: "Kutumia Utajiri wa Madini wa Tanzania katika Kukuza Nishati Jadidifu, Mageuzi ya Kidijitali na Usalama wa Jamii."

Alisema kaulimbiu hiyo imechaguliwa kutokana na umuhimu wa madini katika maendeleo ya teknolojia za kisasa ikiwemo Akili Mnemba (AI), vituo vya kuhifadhi taarifa (Data Centres), magari ya umeme na nishati jadidifu.

“Tunataka kuonesha namna Tanzania inaweza kutumia rasilimali zake za madini kuchochea mageuzi ya kidijitali, kuimarisha usalama wa nishati na kukuza maendeleo ya kijamii na kiuchumi,” alisema Profesa Boniface.

Aliongeza kuwa maadhimisho hayo yatahusisha maonesho ya tafiti na ubunifu, mawasilisho ya kitaaluma, makongamano pamoja na majadiliano ya ushirikiano wa kimkakati yatakayowawezesha washiriki kubadilishana maarifa na kujenga mitandao ya kitaaluma na kibiashara.

Kwa mujibu wa UDSM, maadhimisho hayo yatatoa nafasi kwa watafiti na wabunifu kuonesha suluhisho mbalimbali za kisayansi na kiteknolojia zinazolenga kukabiliana na changamoto za maendeleo nchini katika sekta za madini, nishati, kilimo, afya na uchumi wa kidijitali.

Profesa Boniface alisema chuo kinaendelea kutumia maadhimisho hayo kama jukwaa la kuunganisha taaluma, ubunifu na maendeleo ya taifa kwa kuwafikia wananchi, wawekezaji na wadau mbalimbali wa maendeleo.

"Utafiti na ubunifu ni msingi wa maendeleo endelevu. Tunawaalika Watanzania wote kushiriki katika Maadhimisho ya 11 ya Wiki ya Utafiti na Ubunifu UDSM 2026 ili kujionea kazi na mafanikio ya watafiti na wabunifu wetu," alisema.



Top News