Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limefanya mkutano na wadau wa mazingira tarehe 15 Aprili 2026 katika ukumbi wa Maji House, ndani ya jengo la MWAUWASA jijini Mwanza.
Mkutano huo ulihusisha wadau kutoka mikoa ya Mwanza, Mara na Simiyu, wakiwemo wawekezaji wa migodi, viwanda, wasafirishaji na wachakataji wa taka hatarishi, pamoja na wataalamu elekezi wa mazingira.
Lengo la mkutano ni kukumbusha wadau kuhusu haki na wajibu wao katika kuzingatia Sheria ya Mazingira ya mwaka 2004 na Kanuni zake.
Viongozi wa NEMC waliwasilisha mada mbalimbali zilizolenga kuimarisha uelewa wa utekelezaji sahihi wa Sheria na kuhakikisha shughuli za kiuchumi haziharibu mazingira.
Katika mkutano huo, wawekezaji walisisitizwa kuhakikisha wanafanya usajili na kukamilisha mchakato wa Tathmini ya Athari kwa Mazingira na Jamii (ESIA) kabla ya kuanza miradi yao.
Hatua hii inalenga kulinda mazingira, afya za binadamu na viumbe wengine, pamoja na kuepusha hatua za kisheria dhidi ya miradi isiyozingatia taratibu.
Aidha, wataalamu washauri wa mazingira walikumbushwa kuzingatia maadili ya taaluma yao kwa kutoa taarifa sahihi na kuepuka udanganyifu.
NEMC ilionya kuwa ukiukwaji wa miongozo unaweza kusababisha kufutwa kwa usajili na kuhatarisha usalama wa mazingira na jamii.
Kwa upande mwingine, taasisi za serikali zikiwemo halmashauri zilihimizwa kuimarisha ushirikiano katika kusimamia Sheria za mazingira.
NEMC imeeleza kuwa itaendelea kuandaa mikutano kama hii katika maeneo mengine ili kuongeza uelewa na uwajibikaji kwa maendeleo endelevu ya taifa.
Taasisi za Serikali zilizoshiriki ni pamoja na Ofisi ya Rais, Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali, Halmashaur za wilaya za Mwanza, Bonde la Ziwa Victoria, TBS, jeshi la polisi la zima moto, OSHA, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, TMDA