Spika Zungu Aonya Matumizi ya Lugha za Kudhalilisha Bungeni, Kauli ya Mbunge Lucy Mayenga Kufutwa HansadNa Janeth Raphael MichuziTv - Bungeni Dodoma

Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mussa Azan Zungu, amesisitiza umuhimu wa wabunge kuzingatia kanuni, sheria na maadili ya Bunge kwa kuepuka matumizi ya lugha za matusi au kauli zinazoweza kuwadhalilisha wabunge wenzao wakati wa mijadala ya kibunge.

Akiongoza shughuli za Bunge leo Spika Zungu ameeleza kuwa kauli iliyotolewa na Mbunge Lucy Mayenga ya kusema kuwa “mbunge Sigrada Mligo (CHAUMA) hajitambui” ni kauli ya kuudhi na yenye kudhalilisha mbunge mwingine, jambo ambalo halikubaliki ndani ya chombo hicho cha juu cha kutunga sheria.

Amesema kuwa matumizi ya lugha zisizofaa yanakiuka kanuni za Bunge na yanaweza kuathiri hadhi na heshima ya mijadala ya kitaifa inayofanyika ndani ya ukumbi wa Bunge.

Kutokana na tukio hilo, Spika Zungu alitoa onyo kali kwa wabunge wote, akiwataka kujiepusha na kauli zinazoweza kuleta mvutano au kudhalilisha wenzao, huku akisisitiza kuwa nidhamu na heshima ni msingi muhimu wa uendeshaji wa shughuli za kibunge.

Aidha, aliamuru kauli hiyo iliyotolewa na Mbunge Lucy Mayenga iondolewe kwenye hansadi rasmi za Bunge kwa kuwa imeonekana kwenda kinyume na taratibu na maadili ya chombo hicho.

Katika hatua nyingine, Spika Zungu aliwataka wabunge kuendelea kuzingatia sheria, kanuni na maadili ya kibunge ili kulinda heshima ya Bunge na kuhakikisha mijadala inafanyika kwa ustaarabu na kwa maslahi ya taifa.

Awali, Spika huyo alimwapisha rasmi Mbunge mpya wa Jimbo la Isimani, Emanuela Mtafikikolo Kaganda, ambaye amechukua nafasi iliyoachwa wazi kufuatia kifo cha aliyekuwa Mbunge wa jimbo hilo, William Lukuvi.


Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi ametoa wito wa kutumia Maadhimsho ya Siku ya Mazingira Duniani kukumbuka wajibu wa kuunganisha nguvu katika jitihada za kuhifadhi mazingira, na kuhakikisha matumizi adili ya rasilimali nyingi ambazo Tanzania imejaaliwa kuwa nazo.

Makamu wa Rais ametoa wito huo, alipomwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani, ambayo Kitaifa yamefanyika katika Kituo cha Mikutano cha Jakaya Kikwete mkoani Dodoma.

Amesema baadhi ya mambo muhimu ya kuzingatia katika uhifadhi wa mazingira ni pamoja na kuendelea kutoa elimu kwa umma kuhusu masuala ya mazingira na kuimarisha mfumo wa usimamizi wa taka hususan katika Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa dhana ya uchumi rejeshi, kwa kuwa maeneo mengi bado hali ya usafi haridhishi.

Makamu wa Rais ameongeza kwamba, ni vema kuendelea kubadili mtazamo ili kuziona taka kama fursa ya kiuchumi na kuzitumia kutengeneza bidhaa mbalimbali kama vile mbolea, chakula cha mifugo na bidhaa nyinginezo. Hali kadhalika, kuendelea kutekeleza Mkakati wa Taifa wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia ambapo hadi sasa, matumizi hayo yameendelea kuimarika kutoka 6.9% mwaka 2021 hadi kufikia 28.6% mwaka 2025.

Aidha, Makamu wa Rais amehimiza kuongezwa kwa jitihada za uhifadhi na utunzaji wa mazingira ambapo ameagiza Mamlaka zinazotoa vibali vya ujenzi kuweka sharti na kusimamia ili kila kibali cha ujenzi kinachotolewa kinaambatana na agizo la kupanda miti isiyopungua mitano pamoja na kuzielekeza Mamlaka za Serikali za Mitaa hususan Manispaa na Majiji kuazisha Bustani za kijani na kuhakikisha zinatunzwa ipasavyo.

Pia Makamu wa Rais ameagiza Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania kuhakikisha uwepo wa miche ya miti ya kutosha ili kurahisisha na kuwezesha zoezi la upandaji miti nchini, Mamlaka husika kuimarisha udhibiti wa uharibifu wa maeneo yote yanayopandwa miti pamoja na kuiagiza Ofisi ya Makamu wa Rais kupitia kituo cha Taifa cha kuratibu kaboni kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI), kubainisha misitu inayofaa na kuisajili katika biashara ya kaboni.

Vilevile, Makamu wa Rais ametoa rai kwa Taasisi za utafiti kufanya tafiti kuhusu mimea au viumbe vamizi ambavyo vinazidi kuongezeka na kuathiri mifugo na mimea mingine katika maeneo mbalimbali nchini. Pia ameagiza Mamlaka za Serikali za Mitaa kuimarisha mifumo ya usimamizi wa taka hususan kuanzisha vituo vya kuchakata taka ili kupunguza kiasi cha taka katika madampo na kuchagiza urejelezaji.

Makamu wa Rais ametoa wito kwa kila mwananchi kuwajibika kuhakikisha kwamba suala la utunzaji na usafi wa mazingira, ikiwemo udhibiti wa taka linapewa kipaumbele. Amesema ni vema kutambua suala la ulinzi na uhifadhi wa mazingira halina mbadala, kwa kuwa mazingira ndiyo uhai na uchumi.

Kwa upande wake, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhandisi Hamad Masauni, amesema Uzinduzi wa Programu ya Mageuzi ya Kimkakati ya Mazingira Endelevu Tanzania, itakayotekelezwa kwa kipindi cha miaka mitano (2026 – 2030), imelenga kuchochea matokeo makubwa ya haraka katika kurejesha uoto wa asili, kuimarisha ustawi wa mfumo wa ikolojia pamoja na kutoa huduma za kiikolojia ambazo ni msingi muhimu wa uzalishaji katika sekta mbalimbali za uchumi.

Amesema hatua hizo zitaweza kuchangia katika kufanikisha malengo ya Dira 2050 ambayo inalenga kuifanya nchi kuwa na ustawi wa mazingira na ustamilivu mkubwa wa mabadiliko ya tabianchi. Ameongeza kwamba Programu hiyo, inalenga kuhamasisha upandaji wa miti bilioni mbili kila mwaka, kuongeza matumizi ya nishati safi ya kupikia, kuimarisha usimamizi wa taka, kukuza biashara ya kaboni pamoja na kuongeza ushiriki wa wananchi hususani wanawake na vijana katika uchumi wa kijani.

Maadhimisho hayo, yaliobebwa na kauli mbiu isemayo, “Dira 2050: Tuwajibike Kukijanisha Tanzania” yamehudhuriwa na wadau mbalimbali wa mazingira wa Kitaifa na Kimataifa, Viongozi mbalimbali, Wanafunzi na Wananchi.








 Na Mwandishi Wetu

Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) inaandaa mapendekezo ya  kufanya maboresho ya  Kanuni za Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229, ili kuwezesha wahitimu wa taaluma za Habari, Uhusiano na Mawasiliano kwa Umma kupata ithibati bila sharti la kuwasilisha barua ya mwajiri.

Hayo yamesemwa leo tarehe 05 Juni, 2026 na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa JAB, Wakili Patrick Kipangula, wakati akiwasilisha mada kuhusu “Uhuru wa Vyombo vya Habari katika Enzi ya Kidijiti: Wajibu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari” kwenye Kongamano la Uhuru wa Vyombo vya Habari lililoandaliwa na Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) kupitia Idara ya Sanaa na Taaluma za Habari.

Wakili Kipangula amesema maboresho hayo yanalenga kupanua wigo wa wanufaika wa mfumo wa ithibati kwa kuwajumuisha wahitimu wa taaluma hizo mara tu wanapomaliza masomo yao, hatua itakayowawezesha kuwa tayari kuingia katika soko la ajira au kujihusisha na shughuli za kitaaluma zinazohitaji ithibati wakati wowote.

Amesema kwa sasa Kanuni  za Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229, zinamtaka mwombaji wa ithibati kuwasilisha nyaraka za kitaaluma pamoja na barua ya utambulisho kutoka kwa mwajiri au chombo cha habari, taasisi au jukwaa analopeleka kazi zake za kitaaluma.

Kwa mujibu wa Kipangula, mapitio ya kanuni hizo yatawezesha kuondoa changamoto zinazowakabili baadhi ya wahitimu wapya ambao wanakidhi sifa za kitaaluma lakini bado hawajapata waajiri au taasisi za kuwapatia barua za utambulisho zinazohitajika katika mchakato wa maombi ya ithibati.

Awali kabla ya kumkaribisha Wakili Kipangula kutoa wasilisho Mkuu wa Idara ya Sanaa na Taaluma za Habari katika Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), Dkt. Deograsia Ndunguru, ameikaribisha Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) kuendelea kuimarisha ushirikiano na Chuo hicho katika maeneo mbalimbali, ikiwemo maboresho ya mitaala ya uandishi wa habari ili kuendana na mabadiliko ya teknolojia na mahitaji ya sekta ya habari.

Shule ya Royal Family English Medium Primary School imeendelea kujijengea sifa kubwa baada ya kuibuka kinara kwa kushika nafasi ya kwanza katika Manispaa ya Geita kati ya shule 91 katika mtihani wa Moko ya Kanda ya Ziwa.

Shule hiyo yenye wanafunzi 77 wa darasa la saba walioshiriki mtihani huo wameonyesha kiwango cha juu cha ufaulu ambapo wanafunzi 76 wamepata wastani wa A na mwanafunzi mmoja pekee akipata wastani wa B.

Akizungumza baada ya kutangazwa kwa matokeo hayo Mkurugenzi wa shule Mhandisi Lazaro Philipo amesema mafanikio hayo ni matokeo ya ushirikiano mkubwa kati ya walimu, wazazi na wanafunzi.

Ameishukuru jamii kwa kuendelea kuiamini shule hiyo na kuahidi kuongeza juhudi zaidi ili kuifanya Royal Family kuwa kitovu cha elimu bora na maadili mema nchini.


NA MWANDISHI WETU, DODOMA


Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) na Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Taifa (MCC), Mary Chatanda amesema mageuzi makubwa ya kimaendeleo yaliyofanywa na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan yamekuwa chachu ya vyuo vikuu vya ndani na nje ya Tanzania kumtunuku Shahada mbalimbali za Heshima za Uzamivu.

Chatanda ametoa kauli hiyo Juni 5, 2026, Jijini Dodoma ikiwa ni siku moja imepita tangu Chuo Kikuu cha Urafiki wa Watu wa Urusi (RADN University) kumtunuku Shahada ya Udaktari wa Heshima (Honoris Causa), Jijini Moscow, Urusi.

"Unajua utendajikazi mzuri wa Rais wetu Dk. Samia unaonekana duniani kote, na wengi wanaridhishwa na juhudi kubwa zinazofanywa ana serikali katika kuchochea maendeleo ya nchi. Rais amefanya mageuzi makubwa ya kimaendeleo, na ndiyo maana wenzetu wa Urusi wamemtunuku Shahada ya Udaktari wa Heshima," amesema Chatanda.

Sambamba na hilo, Chatanda amesema katika kila sekta, kuna mabadiliko chanya mengi ambayo yamefanyika ndani ya muda mfupi, ndiyo maana hata mataifa mengine yanatambua kazi nzuri zinazofanyika nchini.

Juni 4, 2026, Chuo Kikuu cha RADN kilimtunuku Rais Dk. Samia Shahada ya Udaktari wa Heshima ikiwa ni njia ya kutambua mchango wake katika mageuzi ya sekta ya elimu, kuimarisha hadhi ya Tanzania kimataifa ikiwemo sekta ya utalii.

Baada ya kutunukiwa Shahada hiyo, Rais Dk. Samia amesema mafanikio hayo si yake pekee yake bali ni juhudi za pamoja kama nchi.

"Shahada hii haihusu mafanikio yangu binafsi, bali ni utambuzi wa mchango wa Watanzania wote katika maendeleo ya Taifa na ushirikiano wa kimataifa. Napokea kwa upole, kama Rais wa Tanzania, mtoto wa Afrika na rafiki wa Russia. Siipokei kwa ajili yangu, bali kwa ajili ya Watanzania," amesisitiza Rais Dk. Samia.

Rais Dk. Samia yupo nchini Urusi kwa ziara ya kikazi, ikiwa ni juhudi za kuimarisha diplomasia ya uchumi na mataifa mengine ili kukuza maendeleo endelevu ya kiuchumi na kijamii nchini.


Balozi wa Finland nchini, Bi. Theresa Zitting (kushoto) na Mkurugenzi wa Misitu na Ufugaji wa Nyuki kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii Bw. Daniel Pancras wakizindua rasmi Muongozo wa Uwekezaji katika Sekta ya Misitu Tanzania wakati wa hafla ya Siku ya Misitu ya Finland iliyofanyika Jijini Dar es Salaam.

UBALOZI wa Finland nchini Tanzania, kwa ushirikiano na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) Tanzania kupitia Mpango wa Ubunifu wa FUNGUO, wameadhimisha Siku ya Misitu ya Finland 2026 yenye kaulimbiu “Kufanya Biashara na Finland.”

Tukio hilo limewakutanisha wafanyabiashara, wawekezaji, taasisi za Serikali, wadau wa maendeleo, wajasiriamali, na wataalamu wa misitu kutoka Finland na Tanzania ili kuimarisha ushirikiano wa kibiashara na ukuaji endelevu katika sekta ya misitu.

Mpango huu ulihusisha mada kuu kuhusu fursa za uwekezaji katika sekta ya misitu Tanzania, mawasilisho kutoka kwa makampuni ya Finland, jukwaa maalumu la kukutanisha , na maonyesho ya ufumbuzi endelevu wa misitu kutoka nchi zote mbili.

Hafla hii pia ilishuhudia uzinduzi wa muongozo maalumu wa uwekezaji katika sekta ya misitu (Tanzania Forest Sector Investment Guide).

Akizungumza juu ya umuhimu wa tukio hilo, Balozi wa Finland Tanzania Theresa Zitting amesisitiza umuhimu wa ushirikiano wa kibiashara wa nchi hizi mbili. “Ushirikiano madhubuti wa kibiashara ni muhimu katika kufungua fursa zote za sekta ya misitu Tanzania. Siku ya Misitu ya Finland inatoa fursa ya kipekee kwa makampuni, wabunifu, na wawekezaji kutoka nchi zote mbili kujenga uhusiano, kubadilishana ujuzi, na kubainifursa za kivitendo za ushirikiano,” alisema Balozi Zitting na kuongeza kuwa tukio hili linaashiria dhamira ya muda mrefu ya Finland katika maendeleo endelevu ya kiuchumi ya Tanzania kupitia uwekezaji, ubunifu, na ushirikiano na sekta binafsi.

Akiwakilisha Serikali ya Tanzania Mkurugenzi wa Misitu na Ufugaji wa Nyuki, Wizara ya Maliasili na Utalii, Bw. Daniel Pancras, ameupongeza mpango huu na kusisitiza jinsi unavyoendana na vipaumbele vya maendeleo vya Tanzania. “Sekta ya misitu ya Tanzania ina fursa nyingi kubwa ambazo bado hazijatumiwa kikamilifu, na Finland imekuwa miongoni mwa wabia wetu thabiti na wenye mchango mkubwa katika kufanikishahili. Uhusiano wa namna hii wa kibiashara wa moja kwa moja ndio hasaunaohitajika ilikutafsiri malengo yetu ya pamoja kuwa ajira, kuongeza thamani, na ukuaji endelevu.”

Taasisi ya Finnpartnership imewasilisha huduma zake kwa washiriki wa Tanzania, ikitengeneza fursa mpya za ushirikiano na makampuni ya Finland na upatikanaji wa mifumo ya ufadhili wa pamoja iliyoundwa kusaidia ukuaji wa biashara na ubia wa kimataifa.

Akizungumza kwaniaba ya FinFund, Naibu AfisaMtendaji Mkuu Minnamari Marttila ameangazia fursa za mageuzi zinazotokana na mikutano ya kibiashara iliyoratibiwa vizuri. “Siku ya Misitu ya Finland inatengeneza mazingira, ambapo makampuni yanaweza kwenda mbalizaidi ya utambulisho tu na kuanza kujenga uhusiano wa maana wa kibiashara kupitia kubadilishana ujuzi, uhamishaji wa teknolojia, uwekezaji, na ushirikiano wa mudamrefu wa kibiashara.”

Kivutio kikuu cha siku hii kimekuwa ni maonyesho ya makampuni yanayofadhiliwa kupitia Mpango wa #GreenCatalyst, ambao unaofadhiliwa na Finland chini ya Mradi wa Ubunifu wa FUNGUO unaomilikiwa na UNDP Tanzania. Mpango huu unakamilisha mradi mkubwa zaidi wa Finland unaojulikana kama FORLAND wenye thamani ya Sh61 bilioni za Kitanzania, ukiimarisha zaidi usaidizi wa ukuaji endelevu na jumuishi katika sekta ya misitu Tanzania.

Kupitia awamu yake ya kwanza ya ufadhili, Mpango wa #GreenCatalyst umewekeza zaidi ya Sh1 bilioni za Kitanzania katika makampuni 14 yanayoendeleza misitu endelevu, usindikaji wa mbao unaoongeza thamani, teknolojiazinazohimili mabadiliko ya tabianchi, na ufumbuzi wa uchumi mzunguko.

Uwekezaji huu unajengwa juu ya dhamira ya muda mrefu ya Finland katika sekta ya misitu Tanzania. Ndani ya kipindi cha miakakumi (10), Finland imewekeza €45 milioni (takribani Sh136.3 bilioni za Kitanzania) katika sekta hii, ikisaidia usimamizi endelevu wa misitu, uendelezaji wa ujuzi, ubunifu, na ushirikiano wa sekta binafsi unaochangia ukuaji wa uchumi na uendelevu wa mazingira.

Akizungumza kwa niaba ya UNDP Tanzania, Meneja wa Mradi wa FUNGUO Joseph Manirakiza aliangazia nafasi ya ushirikiano katika kukuza ubunifu. “Ubunifu unastawi pale ambapo wajasiriamali wanapatasiotu ufadhili, bali pia mitandao, masoko, na ushirikiano. Siku ya Misitu ya Finland ni jukwaa la aina yake ambalo wajasiriamali wetu wa #GreenCatalyst wanalihitaji ili kuunganishwa na kukua,” alisema Manirakiza.

Naye mwakililishi wa FORLAND ambao ni mradi unaojihusisha na misitu, matumizi sahihi ya ardhi na kuongeza thamani katika mazao ya misitu, Bw. Masasa Makwassa aliipongeza Finland kw akuadhimisha siku hii muhimu na kusisitiza kuwa shirika hilo litaendelea kushirikiana na wadau wote kuhakikisha malengo ya mradi huo unotekelezwa kwa pamoja na Tanzania na Finland yanafikiwa.

Na. Jordan Mbwambo, WF, Dodoma,

Serikali imefafanua vigezo vinavyotumika katika utozaji wa Kodi ya Majengo (Property Tax) kupitia Mfumo wa Mita za Umeme za LUKU, hatua inayolenga kurahisisha ukusanyaji wa kodi na kuongeza ufanisi katika usimamizi wa mapato ya ndani.

Hayo yameelezwa bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula (Mb), alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Mhe. Tinnar Andrew Chenge, aliyetaka kujua kigezo kinachotumiwa na Serikali katika kutoza Kodi ya Majengo kupitia Mfumo wa Mita za LUKU.

“Kwa sasa Serikali inatumia viwango mfuto katika kutoza kodi ya majengo kupitia mita za umeme za LUKU. Vigezo vinavyotumika kutoza kodi ya majengo kupitia LUKU ni nyumba ya kawaida ambayo inatozwa shilingi 18,000 kwa mwaka au shilingi 1,500 kwa mwezi na nyumba ya ghorofa ambayo inatozwa shilingi 90,000 kwa kila sakafu kwa mwaka au shilingi 7,500 kwa kila sakafu kwa mwezi,” alisema Mhe. Luswetula.

Aidha, alisema kuwa nyumba za nyasi, udongo, majengo ya huduma za jamii, ibada pamoja na nyumba zinazoishi wazee wenye umri wa miaka 60 na kuendelea hazitozwi Kodi ya Majengo isipokuwa pale majengo hayo yanapotumika kwa shughuli za biashara.

Mhe. Luswetula alisema kuwa utaratibu huo unalenga kuhakikisha mfumo wa utozaji kodi unaendelea kuwa rahisi, wenye ufanisi na unaozingatia makundi maalum yanayostahili msamaha kwa mujibu wa sheria.
Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula (Mb), akijibu swali la Mbunge wa Ilemela, Mhe. Tinnar Andrew Chenge, aliyetaka kujua, kigezo kinachotumiwa na Serikali katika kutoza Kodi ya Majengo kupitia Mfumo wa Mita za Luku, bungeni jijini Dodoma.(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Fedha)

Farida Mangube, Morogoro

Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Morogoro imebaini dosari katika mfumo wa ukusanyaji wa mapato na kufanikisha kurejeshwa kwa zaidi ya Shilingi milioni 69 ambazo zilikuwa hazijakusanywa, hatua inayodhihirisha juhudi za taasisi hiyo katika kulinda mapato ya serikali na kuhakikisha fedha za umma zinatumika kwa ufanisi.

Akizungumza na waandishi wa habari kuhusu utekelezaji wa shughuli za TAKUKURU kwa kipindi cha Januari hadi Machi 2026, Naibu Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Morogoro, Christopher Mwakajinga, alisema kiasi cha Shilingi 69,248,392 kilikusanywa baada ya operesheni maalumu ya kufuatilia makusanyo ya mapato kupitia mashine za POS zinazotumia mfumo wa TAUSI. 

Alisema uchunguzi ulibaini kutokuwiana kwa taarifa za makusanyo kati ya mfumo huo na taasisi za kifedha, hali iliyosababisha kuonekana kwa madeni yasiyo halisi kabla ya dosari hizo kurekebishwa.

 Taasisi hiyo pia ilifuatilia utekelezaji wa miradi minane ya maendeleo yenye thamani ya zaidi ya Shilingi bilioni 2.7 kwa lengo la kuhakikisha thamani ya fedha inapatikana. 

Aliongeza kuwa ushauri wa kitaalamu uliotolewa na TAKUKURU uliwezesha kuokolewa au kurejeshwa matumizi yenye thamani ya zaidi ya Shilingi bilioni 15.7 katika sekta mbalimbali ikiwemo elimu, afya na maji.

Kwa upande wa elimu kwa umma, alisema TAKUKURU iliendesha semina 74, mikutano ya hadhara 19 na kuhamasisha uanzishwaji na uimarishaji wa klabu 100 za kupinga rushwa. Aidha, taasisi hiyo ilipokea malalamiko 94 kutoka kwa wananchi, ambapo 65 yalihusu tuhuma za rushwa na kuanza kufanyiwa kazi, huku 29 yakielekezwa kwa mamlaka husika kwa hatua zaidi.

Aliwataka wananchi kuendelea kushirikiana na TAKUKURU kwa kutoa taarifa za vitendo vya rushwa kupitia namba ya bure 113, simu 0738 150 143 au katika ofisi za taasisi hiyo zilizo karibu nao. Baadhi ya wananchi wa Manispaa ya Morogoro wamepongeza juhudi hizo wakisema zimechangia kuokoa fedha za umma na kuimarisha utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwa manufaa ya wananchi.



Na. OWM (KAM) Dodoma

Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Dkt. Evaline Munisi amekutana na kufanya kikao kazi na Wakurugenzi pamoja na wataalamu wa Idara ya Ajira na Ukuzaji Ujuzi kutoka Ofisi hiyo kwa lengo la kuimarisha utekelezaji wa majukumu, kuongeza ufanisi wa kazi na kuimarisha ushirikiano katika utoaji wa huduma kwa wananchi.

Katika kikao hicho kilichofanyika ofisini kwake Dodoma Juni 04,2026 , Dkt. Munisi ameitaka idara hiyo kuongeza juhudi katika kutangaza fursa mbalimbali za ajira na programu za ukuzaji ujuzi zinazotolewa na Serikali ili kuwafikia Watanzania wengi zaidi na kuwawezesha kunufaika na fursa hizo kwa wakati.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa ubunifu, uwajibikaji na ushirikiano katika utekelezaji wa majukumu ya idara hiyo ili kuhakikisha huduma zinazotolewa zinakuwa na tija, zinawafikia walengwa ipasavyo na kuchangia maendeleo ya kiuchumi na kijamii nchini.

 Dkt. Munisi ameelekeza idara hiyo kuweka mkazo katika uboreshaji wa takwimu za soko la ajira na kufanya tathmini ya mara kwa mara ya mahitaji ya ujuzi katika sekta mbalimbali. Alisema hatua hiyo itawezesha Serikali kuandaa programu zinazoendana na mahitaji halisi ya waajiri na soko la ajira kwa ujumla.

Kwa upande wao, Wakurugenzi wa Idara hizo Bi.Alana Nchimbi na Bi.Jane Sorogo wamemshukuru Naibu Waziri kwa maelekezo na mwongozo alioutoa ambapo wameahidi kuongeza kasi ya utekelezaji wa mipango ya idara, ikiwemo kuimarisha ushirikiano na sekta binafsi, vyuo vya ufundi na taasisi za elimu ya juu ili kuhakikisha vijana wanapata ujuzi unaohitajika sokoni.

Kikao hicho ni sehemu ya jitihada endelevu za Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano kuhakikisha kuwa Sera ya Taifa ya Ajira ya mwaka 2008 inatekelezwa kwa vitendo, changamoto za ajira zinapungua na fursa za kiuchumi zinapanuliwa kwa vijana na makundi mengine katika jamii.




Na Mwandishi Wetu

KAMPUNI ya Oryx Gas Tanzania imeendelea kuhamasisha matumizi ya nishati safi kama sehemu ya mchango wake katika uhifadhi wa mazingira, sambamba na kuunga mkono juhudi za Serikali za kuhakikisha wananchi wanatumia nishati safi ya kupikia ambayo ni salama na rafiki kwa mazingira.

Hayo yamesemwa leo Mei 5,2026 na Meneja Masoko na Mauzo wa Oryx Gas Tanzania Shaban Fundi katika Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani ambapo wafanyakazi wa kampuni hiyo wamefanya usafi katika Soko la Kimataifa la Samaki Feri jijini Dar es Salaam ambapo pia kampuni hiyo imekabidhi vifaa vya kufanyia usafi katika soko hilo.

Fundi amesema kampuni hiyo imekuwa ikitekeleza shughuli mbalimbali nchini kwa lengo la kuhamasisha utunzaji wa mazingira na matumizi ya nishati safi.

“Mbali na kufanya usafi wa mazingira katika soko hilo, Oryx pia tumetoa vifaa vya usafi, vifaa vya kunawia mikono pamoja na vifaa vya kutupia taka ili kuboresha mazingira ya wafanyabiashara na wananchi wanaotembelea eneo hilo.

“Leo tupo hapa Soko la Feri kuadhimisha Siku ya Mazingira Duniani kwa kufanya jambo tofauti. Tumeungana na wateja wetu katika kufanya usafi wa mazingira, kutoa vifaa vya usafi na kuhamasisha matumizi ya nishati safi kwa ajili ya kulinda mazingira yetu kwa vizazi vya sasa na vijavyo,” amesema Fundi.

Aidha, amesema soko hilo ni mfano mzuri wa mafanikio ya matumizi ya gesi badala ya kuni na mkaa, hatua ambayo imechangia kupunguza uharibifu wa mazingira na kuongeza usalama katika eneo hilo.

“Hapo awali matumizi ya kuni na mkaa yalikuwa makubwa sana, lakini sasa mazingira yameimarika, usafi umeongezeka na usalama umeimarika. Tunatoa mwito kwa wananchi kuendelea kuachana na matumizi ya kuni na mkaa na badala yake kutumia gesi ambayo ni salama, nafuu na rafiki kwa mazingira.”

Ameongeza Oryx Gas imeendelea kuhakikisha upatikanaji wa gesi unaimarika nchini kote, mijini na vijijini, ili wananchi wengi zaidi waweze kufaidika na nishati hiyo safi.

Kwa upande wake, Meneja wa Soko la Kimataifa la Samaki Feri Suleiman Mfinanga ameipongeza Oryx Gas kwa kuchagua soko hilo kuwa sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani, huku akieleza hatua hiyo imeonyesha dhamira ya kweli ya kampuni hiyo katika kulinda mazingira na kuboresha shughuli za biashara.

Ameongeza soko hilo ni miongoni mwa masoko makubwa ya samaki nchini, hivyo uwekezaji uliofanywa wa miundombinu ya matumizi ya gesi umekuwa na manufaa makubwa kwa wafanyabiashara na mazingira kwa ujumla.

“Tunawashukuru sana Oryx kwa uwekezaji huu mkubwa wa nishati safi mlioufanya katika soko ambapo mlituwekea tanki kubwa na wafanyabiashara wakaunganishiwa gesi ya kupikia. Mradi huu umechangia kwa kiasi kikubwa kutekeleza sera ya taifa ya matumizi ya nishati safi ya kupikia na kuondoa changamoto zilizokuwa zikitokana na matumizi ya kuni na mkaa,” alisema.

Naye mfanyabiashara katika soko hilo, Mwanahawa Noel, amesema ujio wa Oryx na kampeni zake za mazingira umewapa hamasa wafanyabiashara kuendelea kudumisha usafi wa mazingira na kuvutia wageni zaidi katika soko hilo.

“Tunawapongeza kwa kutukumbuka na kuendelea kutuhamasisha kuweka mazingira safi. Hii inasaidia hata wageni kutoka maeneo mbalimbali na nchi jirani kufurahia mazingira mazuri wanapofika hapa,” amesema.

Kwa upande wake, mfanyabiashara mwingine, Shaibu Ulaya, amesema mradi wa gesi uliotekelezwa na Oryx umeleta mafanikio makubwa katika shughuli za biashara na kuboresha mazingira ya kazi kwa wafanyabiashara wa soko hilo.

Maadhimisho hayo yalitumika pia kuelimisha jamii kuhusu umuhimu wa matumizi ya nishati safi katika kupunguza uharibifu wa mazingira, kulinda afya za wananchi na kuchangia maendeleo endelevu ya taifa.



Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Ndugu Asha-Rose Migiro, leo Ijumaa Juni 5,2026 amefanya mazungumzo na Mheshimiwa Marianne Young, Balozi wa Uingereza nchini Tanzania, katika Makao Makuu ya CCM, Dodoma.

Mazungumzo hayo yalihusu maeneo ya ushirikiano wa maendeleo kati ya Tanzania na Uingereza, kwa kuzingatia vipaumbele vilivyobainishwa katika Ilani ya CCM ya Uchaguzi ya mwaka 2025–2030, Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 pamoja na Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs).

Viongozi hao walijadili fursa za kuendeleza ushirikiano kwenye maendeleo ya kijamii na kiuchumi, hususan katika kuwawezesha vijana na wanawake kupitia elimu, ujuzi, ubunifu na uwekezaji.

CCM inaendelea kuthamini ushirikiano wa kimataifa unaochangia maendeleo endelevu na ustawi wa wananchi wa Tanzania.









Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Umoja wa Wazazi Tanzania wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Ally Salum Hapi, amepokelewa mkoani Shinyanga ambapo katika mkutano wake wa hadhara amewataka viongozi na wanachama wa CHADEMA kuelekeza nguvu zao katika kuwasilisha hoja za maendeleo badala ya kuendelea na malalamiko ya kisiasa.

Hapi amesema kuwa baada ya baadhi ya viongozi wa chama hicho kutoka kifungoni na kuanza tena mikutano ya kisiasa, wananchi walitarajia kusikia sera na mikakati ya kuboresha maisha yao, lakini badala yake wameendelea kusikia lawama na malalamiko yasiyoleta suluhisho la changamoto za wananchi.

Amesisitiza kuwa ushindani wa kisiasa unapaswa kujengwa kwenye hoja, sera na mipango ya maendeleo inayoweza kuinua uchumi, kuongeza ajira na kuboresha huduma za jamii.

Aidha, amewataka wananchi wa Shinyanga kuendelea kuiunga mkono Serikali ya CCM chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan kwa mafanikio yanayoendelea kupatikana katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo nchini.









Na Mwandishi Wetu.

TAASISI ya Maonesho ya Ufugaji wa Nyuki barani Afrika ya Africa Bee Expo, imeialika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa mwenyeji wa Maonesho ya Tano ya Ufugaji wa Nyuki Afrika yatakayofanyika mwaka 2028 na kujumuisha wafugaji wa nyuki kutoka nchi 50.

Mwaliko huo umetolewa Juni 4, 2026 na Mwenyekiti wa taasisi hiyo, Bw. Fatah Ben Chouia wa Algeria, alipokutana na kuzungumza na Balozi wa Tanzania nchini Algeria Mobhare Matinyi, katika ofisi za Ubalozi wa Tanzania jijini Algiers.

Pamoja na mwaliko huo, Bw. Chouia aliwasilisha pia mwaliko wa Tanzania kuwa mgeni rasmi katika Maonesho ya Nne ya Ufugaji wa Nyuki Afrika yatakayofanyika jijini Algiers, Algeria, tarehe 3-6 Septemba, 2026, na kuziomba taasisi za serikali na watu binafsi wa Tanzania kushiriki.

Balozi Matinyi aliishukuru taasisi hiyo kwa kuipa Tanzania heshima ya ugeni rasmi mwaka 2026 na uenyeji mwaka 2028 na kuahidi kwamba Serikali itaifanyia kazi mialiko hiyo kwa manufaa ya sekta hiyo ambayo hutoa fursa ya ajira milioni mbili kwa Watanzania na kuchangia katika pato la taifa.

Bw. Chouia aliipongeza Tanzania kwa kuwa moja ya nchi zenye mafanikio makubwa katika ufugaji wa nyuki na mazao yake barani Afrika na duniani kiasi cha kustahili kuwa mwenyeji wa maonesho hayo barani Afrika kwa mwaka 2028.

Maonesho ya nyuki na mazao yake barani Afrika hujumuisha pia nchi mbalimbali duniani na hutoa fursa ya kukutanisha wajasiriamali, wataalamu na watafiti wa ufugaji wa nyuki katika kongamano la kimataifa la utaalamu wa ufugaji wa nyuki, uhifadhi na uzalishaji wa bidhaa zake.

Kwa mujibu wa taarifa za Shirikisho la Kimataifa la Vyama vya Wafugaji Nyuki (Apimondia), Tanzania ni nchi ya pili barani Afrika na ya kumi duniani kwa uzalishaji asali unaofikia tani 31,000 na pia tani 1,800 za nta kwa mwaka.




MERIDIANBET imeleta ladha mpya kabisa kwa mashabiki wa kasino kupitia Meridian Icy Fruits, sloti ya kwanza ya kisasa kutoka kwenye jiko la ubunifu. Mchezo huu umebeba mchanganyiko maarufu wa matunda, kengele na alama za Lucky 7, lakini safari hii ukiwa umevalishwa mwonekano wa kipekee wa majira ya baridi unaovutia macho na kuongeza burudani.

Kitu kinachoufanya Meridian Icy Fruits kuwa tofauti ni muundo wake wa kisasa pamoja na muziki wa kuvutia unaokufanya ujisikie ndani ya ulimwengu wa ushindi. Kila mzunguko una nafasi ya kukupa furaha mpya huku mandhari ya barafu ikiongeza hisia za kipekee ambazo vijana wengi wanazipenda.

Vilevile, meridianbet wana michezo mingi ya kasino mtandaoni na mechi za kimataifa za kubashiri zenye ushindani mkubwa wa odds. Jiunge leo kwa kutembelea tovuti ya MERIDIANBET au piga *149*10# kisha uanze safari yako ya ushindi.

Iwe ndiyo mara yako ya kwanza kucheza sloti au tayari ni mzoefu wa michezo ya kasino, Meridian Icy Fruits imeundwa kwa ajili yako. Mchezo huu ni rahisi kuuelewa lakini umejaa fursa nyingi za kushinda, jambo linaloufanya kuwa chaguo bora kwa kila aina ya mchezaji.

Ukiwa na mistari 40 ya ushindi, kila raundi inakuwa na msisimko wa hali ya juu. Kadiri alama zinavyopangwa kwenye skrini, ndivyo nafasi za ushindi zinavyoongezeka, na kufanya kila dakika ya mchezo kuwa yenye hamasa na matarajio makubwa.

Na kama hiyo haitoshi, Meridian Icy Fruits imeongezewa mchezo wa kubashiri ushindi ambao unaweza kuongeza zawadi zako na kufanya burudani iwe kubwa zaidi. Ingia Meridianbet leo, jaribu Meridian Icy Fruits, na ujionee baridi ya mchezo huu ikiwasha moto wa ushindi.

Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Kikwete akiongoza Mkutano huo wa Bodi ya GPE.
Mwenyekiti wa Bodi ya Taasisi ya GPE Dkt. Jakaya Kikwete akiwa na viongozi wa Taasisi hiyo wakati wa Mkutano huo wa Bodi. Wa kwanza kushoto ni Bw. Charles North, Naibu Afisa Mtendaji Mkuu wa GPE anayetokea Marekani, Bi. Christine Hogan, Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya GPE anayetokea Canada, na kulia kwake ni Bi. Laura Frigenti, Afisa Mtendaji Mkuu anayetokea Italia.

RAIS Mstaafu Jakaya Dkt. Mrisho Kikwete, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Bodi ya Taasisi ya Kimataifa inayoshughulikia Masuala ya Elimu Duniani (Global Partnership for Education - GPE) ameendelea kuwa kinara katika kuhamasisha jitihada za upatikanaji wa fedha za kugharamia elimu kwa watoto wanaoishi katika mazingira magumu duniani.

Kwa nafasi yake ya Mwenyekiti wa Bodi ya GPE ameongoza Mkutano muhimu wa Bodi hiyo uliofanyika Paris, Ufaransa tarehe 3 - 4 Juni, 2025 ambao pamoja na mambo mengine umejadili mkakati wa GPE kukusanya kiasi cha Dola za Marekani bilioni 15 hadi kufikia mwaka 2030 chini ya Kampeni ijulikanayo kama GPE 2030. Mkutano huo wa Bodi ulihudhuriwa pia na Bi. Éléonore Caroit, Waziri wa Nchi wa Ufaransa anayeshughulikia masuala ya Ubia wa Kimataifa na Maslahi ya Wafaransa waishio Ng'ambo.

Kupitia ubia na ushirikiano kati ya Taasisi ya GPE, nchi wafadhili, mashirika ya kimataifa ya misaada, GPE imelenga kuwarejesha watoto takriban milioni 270 ambao hawapo mashuleni kote duniani, hususan kutokana na sababu mbalimbali. Aidha, fedha zinazokusanywa na GPE hutumika pia kugharamia uboreshaji wa elimu ya awali na ya msingi kwa watoto wanaoishi katika nchi za kipato cha chini na zinazoendelea, hususan watoto wa kike na wale wanaojikuta kwenye mazingira magumu kama vile ya vita, ukame, mafuriko, nk.

Kupitia Kampeni hiyo ya GPE 2030, jumla ya wanafunzi milioni 750 kutoka katika nchi 96 kote duniani watanufaika kupitia uboreshwaji wa mifumo ya elimu, ununuzi wa vitabu vya ziada na kiada, ujenzi na uboreshwaji wa madarasa, maabara, na mafunzo kwa walimu na kuwaongezea ujuzi.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Taasisi ya GPE baada ya Mkutano huo wa Bodi, nchi za Italia na Nigeria ndiyo zitaongoza Kampeni ya kukusanya fedha hizo katika hafla maalumu itakayofanyika tarehe 23 Septemba, 2026 pembezoni mwa Mkutano Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UNGA).

Vilevile, taarifa hiyo imeeleza kuwa licha ya mabadiliko ya sasa ya hali ya kifedha duniani ambapo wafadhili mbalimbali, hususan nchi zilizoendelea, zinabadilisha vipaumbele vyao vya maeneo ya kuelekeza ufadhili, Taasisi ya GPE imeridhishwa na mwitikio mzuri wa nchi wafadhili kama vile Ujerumani, Australia, Ufaransa, nk ambazo tayari zimetangaza michango yao kwa kampeni hiyo. Aidha, taarifa hiyo imeeleza kuwa ni matarajio ya GPE elimu ya msingi itaendelea kuwa kipaumbele katika kipindi hiki cha mpito, huku Taasisi hiyo ikiahidi kuwa Taasisi ya mfano wa kuigwa wa ubia na ushirikiano wa kimataifa kwa kuzileta nchi pamoja kupitia lengo la kuboresha elimu ya msingi duniani.

Balozi wa Tanzania nchini Ufaransa, Said Yakubu alihudhuria katika hafla iliyoandaliwa baada ya Mkutano huo. Ikumbukwe kuwa Tanzania ni moja ya nchi wanufaika wa fedha zinazotolewa na Taasisi ya GPE ambapo hadi sasa imeshapokea zaidi ya Dola za Marekani milioni 207.3 kwa ajili ya kuboresha sekta ya elimu nchini. Aidha, GPE imetenga takriban Dola za Marekani milioni 50 kwa ajili ya Tanzania ikiwa ni mwendelezo wa kuboresha sekta hiyo muhimu.

Top News