Morogoro, Tanzania, 10 March 2026: Miaka ya hivi karibuni, magonjwa yasiyoambukiza yanaendelea kuwa changamoto kubwa kwa afya ya jamii nchini Tanzania. Magonjwa kama shinikizo la damu, kisukari, magonjwa ya moyo pamoja na saratani yanaongezeka kwa kasi, huku wengi wakigundulika wakiwa tayari katika hatua za mwisho za ugonjwa kutokana na kukosekana kwa uchunguzi wa mapema na uelewa mdogo kuhusu kinga na dalili zake.
Kwa mujibu wa takwimu za afya nchini, magonjwa yasiyoambukiza yanachangia takribani asilimia 34 ya vifo vyote nchini Tanzania, jambo linaloonyesha umuhimu wa kuimarisha juhudi za kinga, uchunguzi wa mapema pamoja na elimu kwa jamii kuhusu namna ya kujikinga na magonjwa hayo.
Kwa jamii nyingi, hasa zile zilizo mbali na huduma za afya au zenye changamoto za kifedha, watu wengi huchelewa kufanya uchunguzi wa afya hadi pale hali inapokuwa mbaya zaidi. Hali hii huongeza hatari za kiafya ambazo zingeweza kuzuilika kupitia uchunguzi wa mapema na ushauri wa kitaalamu.
Kwa kutambua umuhimu wa kukabiliana na changamoto hii, sekta binafsi zimeendelea kushirikiana na serikali katika kuboresha upatikanaji wa huduma za afya kwa jamii. Katika kuunga mkono juhudi hizi, Vodacom Foundation Tanzania imeanza zoezi la Kambi ya Matibabu ya Bure kwa ajili ya uchunguzi wa magonjwa yasiyoambukiza kwa wakazi wa Morogoro, ikilenga kuwasogezea wananchi huduma muhimu za uchunguzi, ushauri na elimu ya afya.
Baada ya kufanikisha kambi ya afya ya bure iliyofanyika hivi karibuni Zanzibar iliyohudhuriwa na zaidi ya wananchi 2000 waliopata huduma mbali mbali za uchunguzi wa afya na ushauri wa kitabibu, sasa mpango huo unaelekea Morogoro ili kuwafikia wananchi wengi zaidi.
Kwa kushirikiana na madaktari bingwa kutoka Muhimbili National Hospital, Vodacom Tanzania Foundation inaleta tena huduma za uchunguzi na matibabu bila malipo ili kusogeza huduma muhimu za afya karibu zaidi na wananchi.
Kambi hiyo ya afya itafanyika katika Viwanja vya Shule ya Kilosa Mjini mkoani Morogoro, kuanzia tarehe 10 hadi 13 Machi 2026, ambapo wananchi watapata huduma mbalimbali za uchunguzi ikiwemo shinikizo la damu, kisukari, magonjwa ya moyo pamoja na ushauri wa kitaalamu kuhusu namna ya kujikinga na kudhibiti magonjwa yasiyoambukiza.
Mpango huu ni sehemu ya juhudi za muda mrefu za Vodacom Tanzania Foundation katika kusaidia jamii kupitia huduma za afya, elimu na miradi mingine ya maendeleo, huku ukilenga kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu umuhimu wa uchunguzi wa mapema na kinga dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza.
Akizungumza Katika hafla hiyo, Mkuu wa Wilaya ya Kilosa, Shaka Hamdu Shaka, alipongeza Vodacom Tanzania Foundation pamoja na Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa kuandaa makambi haya ya afya yanayotoa huduma bure kwa wananchi wa Kilosa.
“Tunapenda kuishukuru Vodacom Tanzania Foundation na Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa kuwa mdau muhimu katika sekta ya afya na kwa kuendelea kuleta huduma hizi karibu zaidi na wananchi. Kambi hii ya huduma za afya imeandaliwa kwa kuzingatia jiografia ya eneo hili pamoja na mahitaji halisi ya wananchi’
Akielezea kuhusu mpango huo, Meneja wa Vodacom Tanzania Foundation, Sandra Oswald, alisema kuwa afya bora ya jamii ni msingi muhimu wa maendeleo ya taifa.
“Afya njema ndiyo msingi wa jamii yenye nguvu na tija. Kupitia kambi hizi za matibabu bure tunalenga kuwahamasisha wananchi kuchukua hatua za mapema kuhusu afya zao kwa kufanya uchunguzi, kupata ushauri wa kitaalamu na kujifunza njia bora za kujikinga na magonjwa yasiyoambukiza,” alisema.
Aliongeza kuwa Vodacom Tanzania Foundation itaendelea kushirikiana na wataalamu wa afya pamoja na wadau mbalimbali kuhakikisha huduma za kinga na uchunguzi wa magonjwa yasiyoambukiza zinawafikia wananchi wengi zaidi, hususan wale wanaokabiliwa na changamoto za kifedha au umbali wa huduma za afya.
Mpango huu pia unaendana na malengo ya maendeleo endelevu ya kimataifa, hususan Sustainable Development Goal 3 yanayolenga kuhakikisha afya bora na ustawi kwa wote.
Vodacom Tanzania Foundation inawahimiza wakazi wa Morogoro kujitokeza kwa wingi katika kambi hiyo ili kufanyiwa uchunguzi wa afya na kupata elimu kuhusu namna ya kujikinga na magonjwa yasiyoambukiza, kwani uchunguzi wa mapema na uelewa sahihi ni hatua muhimu katika kujenga jamii yenye afya bora na mustakabali imara.