

Akizungumza katika kongamano hilo lililoandaliwa na Cambridge Judge Business School, University of Cambridge, chini ya kaulimbiu ya “Kujenga Mustakabali wa Afrika: Mitaji, Ubunifu na Ukuaji wa Pamoja wa Bara la Afrika,” Zaipuna aliitumia safari ya NMB kama mfano wa taasisi ya Afrika inayoweza kuvutia mtaji, kuchochea ubunifu na kujenga uaminifu.
“Mustakabali wa Afrika hautaletwa kwetu na wengine; utajengwa na sisi wenyewe kupitia mifumo jumuishi, taasisi zinazoaminika na nidhamu ya kuleta matokeo chanya na endelevu kwa vizazi vijavyo,” alisema.
Zaipuna alieleza mageuzi ya NMB kutoka matawi 97, wateja takribani 600,000 na amana za Sh bilioni 150 mwaka 1997 hadi zaidi ya wateja milioni 10 leo. Alisema kati ya mwaka 2021 na 2025, NMB imewekeza zaidi ya Sh bilioni 230 katika miundombinu ya kidijitali, usalama wa mifumo, teknolojia za kiotomatiki na uwezo wa matumizi ya takwimu, huku zaidi ya asilimia 98 ya miamala yote sasa ikifanyika nje ya matawi kupitia njia za kidijitali na mbadala.
Katika mjadala huo, Mtaalamu wa Fedha (Structured Finance) kutoka AfDB, Eghosa Giwa Osaige, alisema kuimarisha uaminifu na kupunguza gharama za vihatarishi ni muhimu katika kuongeza mtiririko wa mitaji kuelekea Afrika.
Mkurugenzi wa Uwekezaji wa BII, Jumai Hadiza Mohammed, alisema hati fungani za kijamii na uendelevu za NMB zinatoa mfano imara kwa benki za Afrika kuhusu namna ubunifu, ubia na masoko ya mitaji vinavyoweza kufungua uwekezaji kwa kiwango kikubwa.
Mkurugenzi Mtendaji na Afisa Mtendaji Mkuu wa NMB Bank Plc, Ruth Zaipuna, akitoa hotuba kuu katika Cambridge Africa Business Conference 2026 katika Chuo Kikuu cha Cambridge, ambako aliwasilisha safari ya mageuzi ya NMB na mchango wake katika uchumi wa Tanzania.
Na Janeth Raphael -MichuziTv Singida
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Nchemba, ameagiza kuchukuliwa hatua kali za kisheria dhidi ya watumishi wote wa umma watakaobainika kuhusika na ubadhirifu wa fedha za Serikali, akisisitiza kuwa tabia ya kuwahamisha badala ya kuwakamata imekuwa ikichangia kuendelea kwa vitendo vya wizi katika maeneo mbalimbali nchini.
Dkt. Mwigulu ametoa kauli hiyo leo Mei 31, 2026 wakati akizungumza na wananchi wa Itigi mkoani Singida, ambapo ameeleza kuwa Serikali haitavumilia watumishi wanaotumia nafasi zao vibaya kwa kuiba mali na fedha za umma zilizotokana na kodi za wananchi.
Amesema watumishi wanaobainika kufanya ubadhirifu hawapaswi kuhamishwa kutoka kituo kimoja cha kazi kwenda kingine kwani hatua hiyo haina tija, badala yake huwapa nafasi ya kuendelea kufanya vitendo hivyo katika maeneo mapya wanayopelekwa.
“Mwizi wala msimuhamishe. Mkishamhamisha anaenda kuiba na huko. Wale ambao walishahamishwa, kule walikopelekwa RPC wa huko awakamate,” alisema Waziri Mkuu huku akipigiwa makofi na wananchi waliohudhuria mkutano huo.
Katika hotuba yake, Dkt. Mwigulu alionesha kusikitishwa na baadhi ya watumishi wa umma wanaoshindwa kutambua dhamana waliyopewa na wananchi, akibainisha kuwa wengi wao wamepata elimu kwa gharama za Serikali kupitia kodi za Watanzania na baadaye kupewa nafasi za kazi ili kulitumikia taifa.
Amesema ni jambo la kushangaza kuona baadhi yao wakitumia nafasi hizo kwa manufaa binafsi badala ya kuwahudumia wananchi kwa uadilifu na uzalendo.
“Kuna watu hawamwogopi hata Mungu. Umesoma kwa kodi za Watanzania, umepata nafasi ya kuwatumikia wenzako, lakini unaamua kuwaibia. Wakati huo huo kuna vijana wengi wenye sifa wanaosubiri nafasi za ajira,” alisema.
Waziri Mkuu ameongeza kuwa Serikali inaendelea kupambana na vitendo vya rushwa, ubadhirifu na matumizi mabaya ya fedha za umma ili kuhakikisha rasilimali za nchi zinatumika kwa manufaa ya wananchi wote.
Aidha, alihoji mantiki ya kuendelea kuwahamisha watumishi wanaotuhumiwa kwa ubadhirifu huku Serikali ikibeba gharama za uhamisho wao, ikiwemo posho na nauli, jambo alilosema halina tija katika mapambano dhidi ya wizi wa mali za umma.
“Baada ya kuiba unataka tukuhamishe na tukulipie nauli ya kuhama. Hata hizo sheria tutazirejea. Mimi sichukii watu, lakini nachukia wizi,” alisisitiza.
Kauli ya Waziri Mkuu imekuja wakati Serikali ikiendelea kusisitiza uwajibikaji, uwazi na nidhamu katika utumishi wa umma, huku ikitaka fedha za wananchi zilindwe na kutumika ipasavyo kwa ajili ya kuharakisha maendeleo na kuboresha huduma za kijamii nchini.
Wakazi wa Itigi waliohudhuria mkutano huo walimpongeza Waziri Mkuu kwa msimamo wake dhidi ya ubadhirifu, wakieleza kuwa hatua kali dhidi ya wahusika zitasaidia kuongeza uwajibikaji na kuimarisha imani ya wananchi kwa taasisi za umma
Na Janeth Raphael MichuziTv Itigi - Singida
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Nchemba, ameielekeza Sekta ya Ardhi kujitathmini kwa kina na kuchukua hatua za haraka kurekebisha changamoto zinazoikabili, akieleza kuwa imeendelea kuwa chanzo kikubwa cha migogoro katika maeneo mbalimbali nchini.
Akizungumza na wananchi wa Itigi mkoani Singida leo Dkt. Mwigulu amesema kumekuwa na ongezeko la migogoro ya ardhi inayotokana na wizi, udanganyifu na uzembe wa baadhi ya watendaji, hali ambayo imekuwa ikisababisha wananchi kugombana na hata kuvuruga mshikamano wa kijamii.
Amesema migogoro hiyo imekuwa ikiwakosesha wananchi haki zao za msingi na kuathiri maendeleo ya jamii, huku baadhi ya wananchi wakijikuta wakipoteza ardhi zao kutokana na mifumo isiyo na ufanisi pamoja na vitendo vya rushwa vinavyohusishwa na baadhi ya watumishi wasio waadilifu.
Waziri Mkuu amesisitiza kuwa sekta hiyo inapaswa kufanya maboresho makubwa yatakayorejesha imani ya wananchi kwa kuhakikisha haki inatendeka kwa kila mwenye madai halali ya ardhi na kwamba serikali haitavumilia watendaji watakaobainika kushiriki vitendo vinavyozalisha migogoro hiyo.
Aidha, ameeleza kuwa ardhi ni rasilimali muhimu kwa maendeleo ya wananchi na taifa kwa ujumla, hivyo ni lazima isimamiwe kwa uadilifu, uwazi na weledi ili kuondoa malalamiko yanayoendelea kujitokeza katika maeneo mbalimbali nchini.
Dkt. Mwigulu ameonya kuwa migogoro ya ardhi ikiendelea kuachwa bila kutatuliwa inaweza kuathiri umoja wa wananchi na kuleta uhasama usio wa lazima, akisisitiza kuwa kila taasisi inayohusika na usimamizi wa ardhi inapaswa kutekeleza wajibu wake kwa kuzingatia sheria, kanuni na maslahi ya wananchi.
Aidha amewataka viongozi na watendaji wa sekta hiyo kuhakikisha wanashughulikia kwa haraka kero za ardhi zinazowakabili wananchi ili kuimarisha amani, mshikamano na maendeleo ya taifa.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Dkt. Mahmoud Thabit Kombo amekutana na Jumuiya ya Diaspora ya Tanzania wanaoishi katika Jamhuri ya Korea na kuwahimiza kuendelea kuwa mabalozi wazuri wa Tanzania kwa kuitangaza nchi na fursa mbalimbali zilizopo katika sekta za uwekezaji, biashara na utalii.
Akizungumza katika mkutano uliofanyika jijini Seoul, Mei 31, 2026, Balozi Dkt. Kombo alisisitiza umuhimu wa Watanzania wanaoishi nje kuifahamu vizuri nchi wanayoishi, ikiwemo tamaduni zake, lugha, sheria na mifumo ya kijamii ili waweze kujumuika kwa urahisi na kujenga uhusiano chanya unaoweza kuleta manufaa kwa Taifa.
Alifafanua kuwa uelewa wa mazingira ya nchi mwenyeji huwasaidia diaspora kutambua fursa za kiuchumi na kijamii ambazo zinaweza kuwanufaisha wao pamoja na kuimarisha ushirikiano kati ya Tanzania na nchi husika.
Pia aliwahimiza kutumia majukwaa yao mbalimbali ya kitaaluma, kijamii na kibiashara kuitangaza Tanzania pamoja na fursa zinazopatikana katika nchi wanazoishi. Alibainisha kuwa kupitia mitandao na ushirikiano wao, diaspora wanayo nafasi kubwa ya kuvutia wawekezaji, watalii na washirika wa maendeleo kuwekeza na kushirikiana na Tanzania.
Pia alitoa wito kwa Diaspora ambao ni wanafunzi wa elimu ya juu kujikita katika kufanya tafiti zinazolenga kutatua changamoto mbalimbali zilizopo nchini hususan katika sekta za afya, maji, elimu na mazingira.
Kadhalika alitoa rai kwa Diaspora hao kuendelea kudumisha umoja, uzalendo na maadili mema ili kuendeleza taswira chanya ya Tanzania nchini Korea na kimataifa kwa ujumla.
Kwa upande wake, Rais wa Jumuiya hiyo Bi. Eliusta Filikunjombe alieleza utayari wao wa kuendelea kushirikiana na Serikali katika kutangaza fursa na kuimarisha mahusiano ya watu kwa watu kati ya Tanzania na Jamhuri ya Korea.
Awali akizungumza, Balozi wa Tanzania nchini Korea, Mhe. Noel Kaganda alisema idadi ya Diaspora wa Tanzania nchini humo inafikia 300 ambayo inajumuisha wafanyakazi, wafanyabiashara na wanafunzi.
Mhe. Balozi Dkt Kombo yupo nchini Korea kwa ajili ya kushiriki Mkutano wa Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Korea na Afrika.
.jpeg)
Zaidi ya wafugaji 200 wa Kanda ya Ziwa wamepata elimu kuhusu matumizi ya mifumo ya kidigitali katika sekta ya mifugo, iliyotolewa na kampuni ya climb Up Limited, ili kuwawezesha wafugaji kuongeza tija katika uzalishaji wa mifugo bora na kuachana na mbinu za ufugaji ambazo zimepitwa na wakati.
Hayo yameelezwa na Afisa Masoko wa kampuni hiyo, Jackline Cosmas, Mei 31 mkoani Shinyanga wakati wa kuhitimisha Maonyesho ya Mifugo ya Kanda ya Ziwa yaliyofanyika kwa muda wa siku mbili.
Baadhi ya wafugaji waliotembelea banda la Climb Up Limited na kupata mafunzo hayo wamesema elimu waliyoipata itawasaidia kubadilisha mtazamo wao kuhusu ufugaji, kutoka katika mbinu za jadi na kuelekea ufugaji wa kisasa unaotumia teknolojia kwa ajili ya kuongeza uzalishaji na ufanisi.
Na Said Mwishehe,Michuzi TV
HATIMAYE Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi mahiri wa Rais Dk.Samia Suluhu Hassan imetangaza rasmi kwamba kuanzia Julai 1 mwaka huu wa 2025 nchi yetu ya Tanzania itaanza utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Wakati utekelezaji huo ukitarajiwa kuanza tarehe hiyo ya Julai 1, tayari upo msingi imara wa kisera, kitaasisi na kiutekelezaji unaolenga kuharakisha mageuzi ya kiuchumi, kijamii na kiutawala kwa miongo ijayo.
Katika kikao chake kilichofanyika Dar es Salaam hivi karibuni chini ya Mwenyekiti wake, Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, Tume ya Taifa ya Mipango iliidhinisha miongozo na mifumo muhimu ya kusimamia utekelezaji wa Dira 2050 pamoja na kuelekeza kuharakishwa kwa miradi mikubwa ya kimkakati itakayokuwa nguzo kuu ya ukuaji wa uchumi wa Taifa.
Pamoja na kuidhinisha Mwongozo wa Kitaifa wa Mipango, Mwongozo wa Kitaifa wa Uidhinishaji wa Miradi ya Maendeleo, Mwongozo wa Kitaifa wa Ufuatiliaji na Tathmini ya Miradi ya Maendeleo na Mkakati wa Mawasiliano wa Dira 2050, Tume imeweka msisitizo maalum katika utekelezaji wa miradi mikubwa ya uwekezaji inayotarajiwa kuchochea mabadiliko ya kimuundo katika uchumi wa Tanzania.
Miradi hiyo ni pamoja na Mradi wa Kuchakata Gesi Asilia kuwa Kimiminika (LNG), Mradi Unganishi wa Chuma cha Liganga na Makaa ya Mawe ya Mchuchuma, Mradi wa Kabanga Nickel pamoja na Kiwanda cha Usafishaji Kahama, na Mradi wa Magadi Soda wa Engaruka.
Kwa pamoja, miradi hiyo inawakilisha uwekezaji wenye thamani ya zaidi ya shilingi trilioni 120, sawa na takribani dola za Marekani bilioni 47.
Miradi hiyo imeainishwa kama sehemu muhimu ya utekelezaji wa Dira 2050 kwa sababu ina uwezo wa kuvutia uwekezaji mkubwa wa ndani na nje, kuongeza ajira, kuimarisha mapato ya Serikali, kukuza mauzo ya nje, kuongeza matumizi ya teknolojia za kisasa na kuimarisha ushindani wa Tanzania katika uchumi wa kikanda na kimataifa.
Mradi wa LNG unatarajiwa kuwa kichocheo kikubwa cha ukuaji wa sekta ya nishati na mapato ya fedha za kigeni.
Liganga na Mchuchuma vinatarajiwa kuweka msingi wa maendeleo ya viwanda kwa kuongeza uzalishaji wa chuma na nishati nchini. Kabanga Nickel inaipa Tanzania nafasi ya kushiriki kikamilifu katika uchumi wa kijani unaochochewa na ongezeko la mahitaji ya madini muhimu kwa utengenezaji wa betri na teknolojia za nishati safi duniani.
Nayo Engaruka inafungua fursa mpya katika sekta ya kemikali na viwanda vinavyotegemea malighafi za ndani.
Kwa kuzingatia malengo ya Dira 2050 ya kufikia uchumi wa takribani dola trilioni moja, miradi hiyo siyo uwekezaji wa kawaida bali ni injini za mageuzi ya kiuchumi.
Hivyo uamuzi wa Tume ya Taifa ya Mipango wa kuipa kipaumbele utekelezaji wake unaashiria dhamira ya Serikali ya kuhakikisha Dira 2050 inatafsiriwa katika matokeo halisi yatakayoongeza tija, ajira, ustawi wa wananchi na ushindani wa Taifa katika miaka ijayo.
Pamoja na hayo ukweli ni kwamba kuanza kwa utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inaonesha dhamira,kiu na shauku ya Rais Dk.Samia Suluhu Hassan kuona nchi yetu inapiga hatua zaidi katika kuleta maendeleo, kuboresha hali za maisha ya wananchi na kubwa zaidi kuifanya Tanzania kuwa injini ya kukuza uchumi wake kupitia rasilimali zake .
Unapoiangalia Dira ya Taifa ya Maendeleo unaiona Tanzania tuitakayo na safari ya kuelekea huko inaanza sasa. Hongera Serikali ya Awamu ya Sita kwa hatua hii inayowasha taa ya kijani yenye matumaini makubwa kwa Watanzania.
Lakini kwa muda mrefu Watanzania tumekuwa tukiitamani Tanzania itakayokuwa na uwezo mkubwa wa kuajiri watu wake kupitia sekta mbalimbali na katika Dira hiyo imeeleza kwa kina namna ambavyo nchi inavyokwenda kuimarisha sekta hizo kama mkakati wa kutengeneza fursa za ajira kwa Watanzania.
Kwa mfano Tume ya Taifa ya Mipango chini ya Rais Dk.Samia Suluhu Hassan katika kikao chake cha Mei 26 pamoja na mambo mengine pia imeidhinisha sekta za kipaumbele 12 wakati wa utekelezaji wa dira hiyo.
Sekta hizo ni ya kilimo idadi ya viashiria vya upimaji katika mabano ni (15), viwanda na ujenzi (10), Madini na Nishati(10), Utalii(5), michezo na Sanaa(9), sekta ya ubunifu na maudhui ya kidigitali(2) wakati sekta ya miliki ,aridhi na maendeleo ya miji(13)
Pia sekta nyingine ni biashara na uwekezaji(12), Elimu(54), hifadhi za jamii,kazi na ustawi wa jamii(34), uchumi wa bluu(18) pamoja na sekta ya Sayansi,teknolojia,ubunifu na uchumi wa digitali(24).
Unapoangalia sekta hizo ambazo zimepewa kipaumbele katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 utabaini mkakati uliopo kama nchi ni kuhakikisha Tanzania inaendelea kufungua fursa zaidi ambazo kila mmoja atashiriki katika shughuli za kiuchumi na hatimaye kwa pamoja kubadilisha maisha yetu kutoka tuliyonayo sasa na kuwa na maisha bora zaidi.
Na kwa kuwa dira hiyo imelenga kubadilisha maisha yetu ni matumaini yangu wananchi wote na wa rika na kada zote tunaowajibu wa kuungana na Rais Dk.Samia na Serikali anayoiongoza katika kuwa sehemu ya safari ya kutekeleza dira hiyo ambayo ikifanikiwa kizazi kilichopo sasa na kijacho kitakuwa kwenye ile nchi ya ahadi ya asali na maziwa.
Kupitia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inaonesha jinsi ambavyo inakwenda kuinua uchumi wa mtu mmoja mmoja na lengo ni kuwezesha pamoja na kuwa na ukuaji wa uchumi kwa ujumla kama Taifa lakini pia uchumi wa kila mmoja wetu nao ukue.Ndio mpango uliopo.
Binafsi sina shaka na Rais Dk.Samia katika kusimamia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kwani kwa dhamira yake na utashi wake ndio aliyetoa maelekezo ya kuandikwa kwa Dira hiyo kazi ambayo ilifanyika kwa weledi mkubwa na kupita katika hatua mbalimbali na hatimaye sasa utekelezaji wake unakwenda kuanza rasmi.
Hata hivyo nitoe rai kwa Vyama vya siasa nao wanapaswa kuwa sehemu ya kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wa dira hiyo.Ni matumaini yangu kama ilivyo kwa CCM Ilani yake imeakisi kwa kiasi kikubwa yaliyomo katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Hivyo kwa vyama vya siasa vya upinzani kuakisi yaliyomo katika Dira hiyo kupitia Ilani zao.Lakini kwa kuwa utekelezaji wa dira unaanza Julai 1,2026 ni vema wanasiasa wetu bila kujali itikadi ya vyama wakaungana na Watanzania wote kuitekeleza dira hiyo.
Simu 0713833822
Mwisho
Eneo la BEMC lilianzishwa kisheria kupitia Tangazo la Serikali Na. 123 la tarehe 24 Mei 2013. Lina jumla ya hekta 9,800, ambapo hekta 887 zimetengwa mahsusi kwa ajili ya Bandari ya kisasa ya Mbegani. Sehemu iliyobaki, yenye hekta 8,903, inatumiwa kwa shughuli za uwekezaji. Mradi huu unatajwa kuwa wa kimkakati kitaifa na unalenga kukuza sekta ya viwanda, biashara na uchumi kwa ujumla.
Katika Mpango wa Maendeleo wa Taifa, BEMC umetambuliwa kama moja ya nguzo zitakazosaidia Tanzania kufikia lengo la kuwa na uchumi wenye thamani ya dola trilioni moja ifikapo 2050. Kufikia Mei 2026, wawekezaji 24 tayari walikuwa wameshapatiwa maeneo na kuanza utekelezaji wa miradi yao. Miradi hiyo ipo katika hatua tofauti kama ujenzi wa viwanda, mabanda ya uzalishaji, uzio pamoja na miundombinu wezeshi.
Wakati wa ziara hiyo, Kamati ilisema imefurahishwa na kasi ya ujenzi na uwekezaji unaoendelea. Miongoni mwa miradi iliyotajwa kuvutia ni kiwanda cha Sinovest Industry Investment Limited kitakachozalisha nguo na bidhaa za nguo. Kiwanda hicho kimejengwa kwenye eneo la mita za mraba 210,080, sawa na hekta 21. Mpaka Mei 2026, uwekezaji uliofanyika ulifikia dola milioni 7 za Marekani, sawa na zaidi ya shilingi bilioni 21. Kinatarajiwa kuanza uzalishaji rasmi mwishoni mwa Juni 2026.
Kukamilika kwa kiwanda hicho kutaleta ajira nyingi. Awamu ya kwanza itazalisha ajira 1,000 za moja kwa moja, na awamu ya pili itaongeza ajira 500. Kiwanda kitatumia mashine za kisasa kuzalisha nguo zenye ubora wa kimataifa kwa ajili ya masoko ya Marekani na Ulaya.
Uwekezaji wa aina hiyo unachangia kwa kiasi kikubwa pato la Taifa, unaongeza thamani ya bidhaa za viwandani, pamoja na kuboresha kipato cha wananchi wa Bagamoyo, Mkoa wa Pwani na Tanzania nzima.
TISEZA inalenga kuhakikisha maeneo yote maalum ya uwekezaji yanatumika kikamilifu ili kuvutia mitaji na kuleta tija kwa wananchi. Lengo ni kuwafanya Watanzania wanufaike na fursa za uwekezaji katika sekta mbalimbali. Uwekezaji unabaki kuwa chombo muhimu cha kutoa ajira, kuvutia mitaji kutoka nje, kuhamisha teknolojia na kuimarisha msingi wa viwanda nchini.
Maendeleo yanayoonekana BEMC yanaonyesha nia ya dhati ya Serikali katika kuboresha mazingira ya uwekezaji na kusukuma utekelezaji wa miradi mikubwa yenye maslahi mapana kwa wananchi na Taifa.
-Pia yabainisha mkakati wa mageuzi katika mifumo ya utawala na utumishi wa umma
-Utekelezaji Dira 2050 kuanza kutekelezwa rasmi kuanzia Julai 1, 2026
Na Said Mwishehe,Michuzi TV
TUME ya Mipango ya Taifa imeidhinisha miongozo minne itakayotumika katika kusimamia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 utakaoanza Julai 1 mwaka 2026.
Akizungumza leo Mei 31 katika mkutano wa waandishi wa habari uliofanyika Ikulu jijini Dar es Salaam,Waziri wa Mipango na Uewekezaji Profesa Kitila Mkumbo amesema miongozo hiyo imetolewa baada ya Tume ya Taifa ya Mipango chini ya Mwenyekiti wake Rais Dk.Samia Suluhu Hassan kufanya kikao Mei 26 mwaka huu.
“Katika kikao hicho, pamoja na mambo mengine, Tume ya Taifa ya Mipango ilijadili na kuidhinisha miongozo/mikakati minne itakayotumika katika kusimamia tekelezaji wa Dira 2050 utakaonza Julai 1, 2026.”
Profesa Mkumbo ameitaja miongozo hiyo ni Mwongozo wa Kitaifa wa Mipango,Mwongozo wa Kitaifa wa Uidhinishaji wa Miradi ya Maendeleo, Mwongozo wa Kitaifa wa Ufuatiliaji na Tathmini ya Miradi ya Maendeleo,Mkakati wa Mawasiliano wa Dira 2050 wa Miaka Mitano 2026/27 - 2030/31.
“Ilipojadili Muongozo wa Kitaifa wa Ufuatiliaji na Tathmini ya Miradi ya Maendeleo, Tume ya Taifa ya Mipango iliidhinisha maeneo makubwa matatu ya kimkakati yanayohitaji mageuzi yenye viashiria vya upimaji 142.
“Maeneo haya na idadi ya viashiria vyake ya upimaji ni Mageuzi katika mifumo ya utawala na utumishi wa umma (Governance and civil service reforms, viashiria 13), Mageuzi katika uwekezaji na uzalishaji (structural transformation for investment, infusion and productivity, viashiria 53) pamoja na Mageuzi katika maendeleo ya kijamii, kiuchumi na mazingira (socio economic outcomes, viashiria 76)
Ameongeza pia Tume ya TaĆfa ya Mipango ilidhinisha sekta za kipaumbele 12 kama zilivyainishiwa katika Mpango wa Nne wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano yenye viashiria vya upimaji 206
Amefafanua katika sekta ya kilimo idadi ya viashiria vya upimaji katika mabano ni 15, viwanda na ujenzi (10), Madini na Nishati(10), Utalii(5), michezo na Sanaa(9), sekta ya ubunifu na maudhui ya kidigitali(2) wakati sekta ya miliki ,aridhi na maendeleo ya miji(13)
Pia katika sekta ya biashara na uwekezaji(12), Elimu(54), hifadhi za jamii,kazi na ustawi wa jamii(34), uchumi wa bluu(18) pamoja na sekta ya Sayansi,teknolojia,ubunifu na uchumi wa digitali(24).
Akieleza zaidi Profesa Mkumbo ameeleza pia Tume ya Taifa ya Mipango ilielekeza kuwa Sekretariati ya Tume ijielekeze na kujikita katika kusimamia utekelezaji wa mipango ya maendeleo.
Aidha, katika kumarisha simamizi wa utekelezaji wa mipango ya maendeleo, Mwenyekiti wa Tume alielekeza kuwa, wakati ambapo Tume haikutani katika vikao vya kawaida chini yake, wajumbe wa Tume watajigeuza kuwa Ofisi ya Usimamizi wa Utekelezaji wa Mipango (Delivery Bureau) na vikao vyake vitasimamiwa na Makamu Mwenyekiti wa Tume.
Ameongeza Tume ya Taifa ya Mipango ilielekeza kukamilishwa kwa haraka kwa majadiliano kati ya Serikali na wawekezaji kuhusu miradi ya kimkakati ya uwekezaji inayotarajiwa kujenga msingi ya kukuza uchumi na kuchochea ajira kama sehemu muhimu ya utekelezaji wa Dira 2050 na Mpango wa Nne wa Taifa wa Maendeleo ya Miaka Mitano (2026/27 - 2030/31).
Amitaja miradi hiyo ni Mradi unganishi wa chuma cha Liganga na makaa ya mawe ya Mchuchuma, Mradi wa magadi soda wa Engaruka, Mradi wa kuchakata gesi asilia kuwa kimiminika (LNG), Mradi wa nikeli wa Kabanga (Kabanga Nickel Project) na kiwanda cha usafishaji cha Kahama.










































.jpeg)
