Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma 

CRDB Bank kupitia Kitengo chake cha Manunuzi (Procurement) imetembelea Makao ya Taifa ya Kulelea Watoto yaliyopo Kikombo, Ihumwa jijini Dodoma, na kutoa msaada wa mahitaji muhimu kwa watoto wanaolelewa katika kituo hicho, ikiwa ni sehemu ya juhudi zake za kuimarisha ustawi wa jamii.

Akizungumza mara baada ya kuwasili katika kituo hicho, Mkuu wa Manunuzi – Mikataba, Udhibiti na Uzingatiaji wa CRDB Bank, Victor Mukami, amesema lengo la ziara hiyo ni kujionea hali halisi ya maisha ya watoto hao, kujifunza pamoja na kusikiliza changamoto zinazowakabili.

Ameeleza kuwa hatua hiyo ni sehemu ya mkakati mpana wa benki hiyo wa kuhakikisha inabaki kuwa karibu na jamii, wadau wake pamoja na makundi yenye uhitaji, kupitia utekelezaji wa sera ya kurejesha kwa jamii (Corporate Social Responsibility – CSR).

“Tumekuja hapa Kikombo kuona kwa karibu hali halisi ya kituo hiki katika ngazi ya kitaifa, kujifunza na kubadilishana mawazo. Hii si mara ya mwisho, tutaendelea kutembelea vituo mbalimbali nchini,” amesema Mukami.

Aidha, Mukami ametoa wito kwa wadau mbalimbali kujitokeza kusaidia vituo vya kulelea watoto, akisisitiza kuwa bado kuna mahitaji makubwa yanayohitaji ushirikiano wa pamoja kutoka kwa jamii.

Pia amewasihi wazazi na walezi kuendelea kuwaonesha watoto upendo na malezi bora, akibainisha kuwa upendo una mchango mkubwa katika ukuaji wao wa kiakili na kisaikolojia.

Kwa upande wake, Meneja wa Makao hayo, Darius Karijongo, ameishukuru CRDB Bank kwa msaada huo, akisema kuwa ujio wao umeleta faraja kubwa kwa watoto pamoja na uongozi wa kituo hicho.

“Tunawashukuru sana CRDB Bank kwa kujitokeza kutuunga mkono. Hawa watoto wanahitaji upendo ambao hawakupata kutoka kwa familia zao za karibu. Sisi sote ni familia yao sasa,” amesema Karijongo.

Ameongeza kuwa msaada uliotolewa una thamani kubwa kwa maendeleo ya kituo hicho, na kuahidi kuwa utatumika ipasavyo kwa manufaa ya watoto hao.

“Leo mmetuonesha kuwa ninyi ni ndugu zetu wa karibu. Tunawashukuru sana kwa zawadi mlizotupatia, Mungu awabariki,” ameongeza.

Ziara hiyo inaonesha dhamira ya dhati ya CRDB Bank katika kuendelea kugusa maisha ya Watanzania na kuchangia maendeleo ya jamii kwa ujumla.





 

Na Mwandishi Wetu,Nzega

Halmashauri ya Wilaya ya Nzega mkoani Tabora imeipongeza Kampuni ya Tumbaku ya Alliance One kwa kuwa kinara wa juhudi za upandaji miti ili kurejesha misitu iliyoharibiwa kutokana na shughuli za kibianadamu wilayani humo.

Akiongea katika hafla ya upandaji miti iliyoadaliwa na Kampuni hiyo katika shule ya msingi Ngukumo na Ikiniziwa, Mwakilishi wa Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Nzega Farida Hamis amesema mchango wa Alliance One ni muhimu katika kufanikisha maelekezo ya Rais Samia Suluhu Hassan yanayoitaka kila Halmashauri kupanda miti milioni 1.5 kila mwaka.

Bi. Hamis amesema kuwa Wilaya ya Nzega imekuwa miongoni mwa maeneo yaliyoathirika kwa kiasi kikubwa na uharibifu wa misitu kutokana na shughuli za kibinadamu, hususan ukataji miti kwa ajili ya kuni, uchomaji mkaa pamoja na shughuli za ukaushaji wa tumbaku.


Amesema juhudi za Kampuni ya Alliance One zimekuja wakati muafaka katika kurejesha uoto wa asili na kulinda mazingira kwa vizazi vya sasa na vijavyo.

Ameeleza kuwa ushirikiano kati ya Halmashauri na Kampuni hiyo umeongeza kasi ya upandaji miti pamoja na utoaji wa miche katika maeneo mbalimbali, hususan mashuleni, hatua inayosaidia kujenga msingi wa mabadiliko ya tabia kwa jamii kuanzia kwa wanafunzi.

“Kupitia wanafunzi hawa, tunajenga kizazi chenye uelewa wa thamani ya mazingira, ambacho kitaendelea kutunza miti hii hadi ikue na kutoa manufaa,” amesema.

Kwa upande wake, Mratibu wa masuala ya miti kutoka Kampuni ya Alliance One, Rashid Salum, amesema kampeni ya upandaji miti ilianza mwaka 2023 ikiwa na lengo la kurejesha misitu iliyoharibiwa na kuhakikisha upatikanaji endelevu wa kuni hususan katika sekta ya tumbaku.

Amesema kuwa hadi sasa, kampuni hiyo imefanikiwa kupanda miti katika eneo la hekta 818 wilayani Nzega, huku pia wakipanua juhudi hizo katika Wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma ambapo zaidi ya hekta 800 zimepandwa miti.

Ameongeza kuwa wanashirikiana kwa karibu na Halmashauri pamoja na wananchi wa maeneo husika, ambapo baadhi yao hupata ajira za muda kupitia shughuli za upandaji na utunzaji wa miti.

Salum amesisitiza kuwa moja ya mikakati yao mikubwa ni kuhakikisha miti inayopandwa inalindwa na kukua, ndiyo maana wameanza kuhusisha wanafunzi wa shule za msingi na sekondari ili kujenga tabia ya kuitunza.

“Kwa leo hii tumepanda miche 300 katika Shule ya Msingi Ngukumo na miche 200 katika Shule ya Sekondari Ikiniziwa. Wanafunzi wenyewe kwa kushirikiana na walimu wao wameipanda, jambo linalowajengea uwajibikaji wa kuitunza hadi ikue,” amesema.

Ameongeza kuwa kampeni hiyo ni endelevu katika maeneo yote yanayozalisha tumbaku, ili kuhakikisha kuwa kunakuwepo na rasilimali ya kuni ya uhakika bila kuendelea kuharibu misitu ya asili. Pia ametoa wito kwa wananchi kuendelea kupanda miti katika maeneo yao binafsi ili kuongeza juhudi za uhifadhi wa mazingira.

Kwa upande wao, wanafunzi wa Shule ya Msingi Ngukumo, Sada Maganga na Baraka Amoni, wameishukuru Kampuni ya Alliance One kwa kuwapatia miche ya miti na kuwashirikisha moja kwa moja katika zoezi la upandaji.

Wamesema kuwa wamejifunza umuhimu wa miti katika kuhifadhi mazingira na wameahidi kuitunza miti waliyoipanda ili iweze kukua na kuleta faida kwa shule yao na jamii kwa ujumla. “Tutailinda miti hii kwa sababu tumejua umuhimu wake. Itatupatia kivuli, hewa safi na hata kuni hapo baadaye,” wamesema kwa pamoja.

Hatua hiyo inaonekana kuwa mwanzo wa mabadiliko chanya ya kimazingira wilayani Nzega, huku ushirikiano kati ya sekta binafsi, Serikali na jamii ukiendelea kuwa nguzo muhimu katika kufanikisha uhifadhi endelevu wa misitu.

Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Nzega Bi Farida Hamis akipanda moja ya miti katika shule ya msingi Ngukumo wilayani Nzega, miti ambayo imetolewa na kampuni ya Tumbaku Alliance One kwa ajili kuchangia zoezi upandaji miti milioni 1.5 wilayani humo sambamba na agizo la serikali.

Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Ngukumo wilayani Nzega,Bw Edmund Sinkonda, akipanda moja ya miti iliyotolewa na kampuni ya Tumbaku Alliance One kwa ajili kuchangia zoezi upandaji miti milioni 1.5 wilayani humo sambamba na agizo la serikali.
Batuli Hemedi Mtendaji wa Kijiji cha Ngukumo wilayani Nzega akipanda moja ya miti iliyotolewa na kampuni ya Tumbaku Alliance One kwa ajili kuchangia zoezi upandaji miti milioni 1.5 wilayani humo sambamba na agizo la serikali.
Mwanafunzi wa Darasa la Sita katika shule ya Msingi Ngukumo wilayani Nzega, Lucia Fidelis, akipanda mmoja ya miti shuleni hapo miti iliyotolewa na kampuni ya Tumbaku Alliance One kwa ajili kuchangia zoezi la upandaji miti milioni 1.5 wilayani humo sambamba na agizo la serikali.

Baraka Amon, Mwanafunzi wa darasa la sita katika shule ya msingi Ngukumo wilayani Nzega, akipanda moja ya miti iliyotolewa na kampuni ya Tumbaku Alliance One kwa ajili kuchangia zoezi upandaji miti milioni 1.5 wilayani humo sambamba na agizo la serikali.


Mkuu wa wilaya ya Ukerewe, Mhe. Christopher Ngubiagai (aliyesimama),akizungumza wakati akifungua mafunzo kwa waganga wa tiba asili na tibambadala yaliyoandaliwa na Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu waSerikali. Mafunzo hayo yalifanyika kwa siku mbili kuanzia Machi 26 hadi 27, 2026. Kulia ni Meneja wa Ofisi ya Kanda ya Ziwa, John Wanjala na kushotoni Kaimu Meneja wa Maabara ya Chakula na Dawa, Everlight Matinga.

*************

 

Serikali kupitia Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali imeendelea kuonesha dhamira ya kuinua sekta ya tiba asili nchini baada ya kuzindua mafunzo ya uchakataji salama wa dawa asili kwa waganga wa tiba asili na tiba mbadala kutoka mikoa ya Mara, Simiyu na Mwanza.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo yaliyofanyika Machi 26, 2026 Ukerewe, Mkuu wa Wilaya ya Ukerewe, Christopher Ngubiagai, alisema serikali inatambua mchango mkubwa wa waganga wa tiba asili katika utoaji wa huduma za afya kwa Watanzania, huku akisisitiza kuwa mafunzo hayo ni sehemu ya utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Afya inayotambua rasmi tiba asili na tiba mbadala hapa nchini.

“Serikali imewaleta wataalamu wa GCLA ili kuhakikisha dawa za asili zinachakatwa kwa viwango vinavyokubalika, zinakuwa salama na zenye ubora unaoweza kushindana hata katika masoko ya kimataifa,” alisema Ngubiagai.

Aidha, Ngubiagai Aliongeza kuwa jitihada hizo pia zinalenga kurasimisha sekta ya tiba asili na kuwajengea uwezo waganga hao ili waweze kuwa sehemu ya mfumo rasmi wa huduma za afya nchini, hatua itakayoongeza heshima na uwajibikaji wao katika jamii, ambapo pia alihusisha mafunzo hayo na Dira ya maendeleo ya Taifa ya mwaka 2050, akibainisha kuwa tiba asili ina mchango mkubwa katika kujenga Taifa lenye watu wenye afya bora, kukuza uchumi shindani unaotumia rasilimali za ndani pamoja na kuchochea ubunifu na ajira.

Katika hatua nyingine, Ngubiagai alisisitiza umuhimu wa kuzingatia misingi ya uchakataji salama ikiwemo usafi wa mazingira ya utayarishaji, matumizi ya vipimo sahihi vya dawa, ufungashaji bora pamoja na ushirikiano na wataalamu wa afya ili kuepuka madhara kwa watumiaji huku akiweka wazi kuwa tiba asili inaweza kuwa chanzo kikubwa cha mapato kupitia biashara na hata utalii wa tiba endapo ubora wake utaimarishwa na kuwekewa viwango vinavyokubalika kitaifa na kimataifa.

Akimwakilisha Mkemia Mkuu wa Serikali, Dkt. Fidelice Mafumiko, Meneja wa Kanda ya Ziwa, John Wanjala, alisema kuwa lengo la Mamlaka ni kuhakikisha dawa zote zinazozalishwa zinakuwa salama, bora na zenye uwezo wa kushindana katika soko la ndani na nje ya nchi huku akieleza kuwa mafunzo hayo yanalenga kuwasaidia waganga wa tiba asili kuendana na mabadiliko ya sayansi na teknolojia, ikiwa ni pamoja na kuboresha uzalishaji na kupanua masoko ya bidhaa zao.

“Popote walipo waganga wa tiba asili, Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali tutaendelea kuwafikia kwa mafunzo na huduma za kitaalamu ili kuhakikisha wanatoa huduma zilizo bora na salama kwa jamii,” alisema Wanjala.

Kwa upande wake Katibu wa chama cha Tiba Asili na Tiba Mbadala (TAMESOT), Maneke Malegeli, akizungumza kwa niaba ya washiriki, aliishukuru Mamlaka kwa mafunzo hayo kwa kuwa yamewasaidia kupata uelewa wa mbinu bora za utengenezaji, utayarishaji na ufungashaji wa dawa asili kwa kuzingatia viwango vinavyolinda afya za watumiaji na kuongeza kuwa mafunzo hayo pia yatawasaidia kujitofautisha na matapeli wanaotumia jina la tiba asili vibaya, huku pia akiiomba Mamlaka kuendelea kutoa elimu hiyo ili iweze kuwafikia waganga wengi zaidi nchini.

Waganga wa tiba asili na tiba mbadala kutoka Ukerewe, wakimsikilizamgeni rasmi (hayupo pichani) wakati akifungua mafunzo hayo ya siku mbili.
Meneja wa Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali, Ofisi ya Kanda ya Ziwa, John Wanjala, akiwasilisha mada kuhusu mbinu bora za uzalishaji na usafi wa dawa za tiba asili kwenye mafunzo yaliyofanyika Ukerewe, mkoani Mwanza.
Mkuu wa wilaya ya Ukerewe, Mhe. Christopher Ngubiagai (katikati), akipokea zawadi kutoka kwa Mlezi wa Waganga na Wakunga wa Tiba Asili - Ukerewe, Makubi Makubi baada ya ufunguzi wa mafunzo hayo.
Mtumishi wa Mamlaka, Lulu Kiwia, akifafanua jambo kuhusu aina yauchunguzi wa kimaabara unaofanyika kwenye dawa asili wakati wamafunzo kwa waganga wa tiba asili na tiba mbadala yaliyofanyika wilayaniUkerewe.
Kaimu Meneja wa Maabara ya Chakula na Dawa, Everlight Matingaakiwasilisha mada kuhusu vifungashio vya dawa asili.
Mshiriki wa mafunzo, Consolata Nabina, akichangia hoja kuhusuufangushaji na uhifadhi wa dawa wakati wa mafunzo hayo yaliyofanyikaUkerewe.

Katibu wa Chama cha Tiba Asili na Tiba Mbadala (TAMESOT), ManekeMalegeli, akiandika maelekezo kutoka kwa Mkuu wa Wilaya (hayupopichani) wakati akifungua mafunzo hayo yaliyofanyika Ukerewe, Mwanza.
Mkuu wa wilaya ya Ukerewe, Mhe. Christopher Ngubiagai (katikati), akiwana viongozi kutoka Mamlaka pamoja na washiriki wa mafunzo ya uchakatajisalama wa dawa asili, waganga wa tiba asili na tiba mbadala mara baada yakufungua mafunzo kwa wataalam hao wa tiba asili na tiba mbadala.
Na Mwandishi Wetu

NAIBU Waziri wa Afya, Dk Florence Samizi amewataka watanzania kuwekeza kwenye miundombinu ya afya ili kusogeza huduma za matibabu karibu na wananchi.

Naibu Waziri ameipongeza hospitali ya E.M ya Kigamboni kwa uwekezaji mkubwa iliyofanya kwenye mtambo wa kisasa wa uchunguzi wa magonjwa CT SCAN na huduma za usafishaji wa damu (Dialysisi) ambao unasaidia kupunguza rufaa zisizo za lazima.

Alitoa pongezi hizo jana Dar es Salaam na wakati wa uzinduzi rasmi wa mashine ya kusafisha damu na mashine ya uchunguzi wa afya CT SCAT ya hospitali hiyo iliyoko kata ya Mjimwema Kigamboni.

Alisema uwekezaji kama huo unasaidia jitihada za serikali kupeleka huduma karibu na wananchi na kuepusha muda na gharama za wananchi kufuata huduma hizo maeneo ya mbali na maeneo wanakoishi.

“Kwaniaba ya Waziri wa Afya Mohamed Mchengerwa napenda kuwapongeza kwa dhati kabisa kwa uwekezaji huu, nilipofika pale nje nilimwambia msaizidi wangu kumbe kitu chenyewe ni kikubwa hivi, nawapongeza sana kwa uongozi mkubwa na kutimiza ndoto na kuwa na wataalamu wazuri maana ungewekeza bila wataalamu isingesaidia sana,” alisema

Alisema uwekezaji uliofanywa na hospitali ya E.M unaonyesha dhamira ya dhati ya kuokoa maisha ya watanzania kupata tiba sahihi na kwa wakati.

“Kama alivyosema Mkurugenzi Mtendaji wa hospitali hii uwekezaji huu umegharimu shilingi bilioni 10 si pesa kidogo ni uwekezaji mkubwa sana tena umefanywa na mtanzania mzawa kusaidia juhudi za serikali kuhudumia watanzania,nawapongeza wote kwa kutimiza haya maono,” alisema

Alisema ili mtu aweze kufanyakazi vizuri lazima awe na afya njema hivyo serikali itaendelea kuwekeza kwenye sekta ya afya kuhakikisha taifa lake linakuwa na wananchi wenye afya.

“Kwa dhati kabisa nampongeza Rais Samia kwa kuwekeza kwenye sekta ya afya, ndani ya miaka minne tu amewekeza zaidi ya trilioni sita ambazo zimeenda kwenye miradi ya ujenzi wa hospitali na zahanati, ameweza kujenga hospitali 119, vituo vya afya 649 na zahanati 2,700 na kuweka vifaa tiba vya kisasa na ameajiri watumishi wa afya,” alisema

“Huduma kama uchujaji wa damu ni muhimu sana kwa wananchi wanaosumbuliwa na figo hivyo huduma hiyo itawasaidia sana wananchi kuchuja damu na kuendelea na maisha yao, huduma hizi tumezoea kuzipata nje ya nchi sasa leo hii mzawa amezileta Kigamboni,” alisema

“Nasikia ni ya kwanza Kigamboni kutoa huduma hii napenda kuwaambia wananchi hakuna haja ya kwenda mbali kutafuta huduma mfike hapa E.M kupata huduma hizo badala ya kuhangaika kwenda mbali,” alisema

Mkurugenzi wa Hospitali hiyo, Dk Egna Makwabe alisema wamekuwa wakipata wagonjwa kutoka nchi za Congo DCR, Zambia, Malawi, Comoro, Burundi Rwanda, Benin, Ghana, Nigeria, Kenya, Urusi china na Marekani .

“Ujio wa wagonjwa kutoka nje ya nchi ulitushangaza sana tunakiuliza je wanakuja kwasababu ya eneo tulilopo au ninini hasa kimewavutia kuacha hospitali zote kuja kwetu tukagundua kuwa ni imani yao kutokana na huduma tunazotoa,” alisema

Alisema kwa sasa hospitali hiyo inahudumia wagonjwa wa nje wastani wa 300 kwa siku na kwamba kwa sasa wanamadaktari bingwa bobezi wauguzi na wataalamu wa maabara.

Alisema E.M itashirikiana na serikali kuhakikisha bima ya afya kwa wote inawanufaisha wananchi wanapougua wasilazimike kutoa fedha kupata matibabu na kwamba walishiriki kutoa maoni kwenye uandaaji wa bima ya afya kwa wote.

Alisema wanatoa huduma za kuwaona wagonjwa wa nje, wanaolazwa, huduma za upasuaji, huduma za matibabu ya mgongo, mfumo wa fahamu na mifupa, huduma za maabara na geologia, huduma za uangalizi maalum na huduma za kibingwa za figo na saratani.

Alisema hospitali imewekeza kwenye huduma za kuchuja damu, mitambo ya kuchunguza magonjwa kama CT SCAN na upasuaji wa kisasa kwa njia ya matunda na karibuni wataanzisha huduma za macho .



Balozi wa Italia nchini Tanzania, Giuseppe Sean Coppola, amesema kuwa Italia inaadhimisha toleo la 10 la Siku ya Ubunifu wa Italia Duniani, tukio linalolenga kuonesha mchango wa nchi hiyo katika ubunifu wa kimataifa.

Amesema mpango huo umeanzishwa na Wizara ya Mambo ya Nje pamoja na Wizara ya Utamaduni ya Italia, ukiwa na lengo la kukuza ubunifu unaochangia maendeleo ya kijamii na kiuchumi duniani.

Akizungumza wakati wa maadhimisho hayo, Balozi Coppola alieleza kuwa Italia ni miongoni mwa mataifa vinara katika ubunifu wa bidhaa, akitaja mji wa Milan kuwa kitovu cha ubunifu barani Ulaya na duniani kwa ujumla.

Kwa mwaka huu, maadhimisho hayo yanaongozwa na kaulimbiu isemayo “Kubuni upya: kurejesha, kuboresha na kubadili mawazo, maeneo na mahusiano.”

Maonesho hayo yanafanyika katika ukumbi wa Rangy Gallery, yakihusisha mradi wa pamoja wa utengenezaji wa vioo kati ya Shanga uliopo Arusha na eneo la Murano nchini Italia.

Mradi huo unahusisha wataalamu wa vioo kutoka Murano waliokuja Tanzania kufundisha mbinu za kisasa za utengenezaji wa bidhaa za mikono. Bidhaa hizo hutengenezwa kwa kutumia taka (recycling), hatua inayochangia uhifadhi wa mazingira.

Aidha, Shanga ni taasisi inayowaajiri watu wenye ulemavu, hivyo kuwa na mchango mkubwa katika maendeleo ya kijamii na kuwainua kiuchumi.

Katika kuimarisha ubunifu huo, Balozi Coppola alibainisha kuwepo kwa ushirikiano na Nelson Mandela African Institution of Science and Technology, unaolenga kulinda haki miliki za wabunifu.

Maonesho hayo pia yanajumuisha bidhaa za vioo kutoka Venice, jiji lenye historia ya zaidi ya miaka 1,000 katika utengenezaji wa vioo, pamoja na taa za kisasa kutoka kampuni ya Potcerini.

Balozi huyo alisisitiza kuwa ubunifu wa Italia unalenga kuunganisha uzuri na matumizi bora (comfort), huku ukimweka mwanadamu katikati ya kila bidhaa inayobuniwa.

Amewahimiza Watanzania kutembelea maonesho hayo yanayoendelea mwezi mzima wa Aprili, pamoja na kuunga mkono bidhaa za ubunifu na miradi ya kijamii kama Shanga.

Akizungumzia mafanikio ya mradi huo, Balozi Coppola alisema kuwa mapokezi yake katika Murano yalikuwa chanya, huku mafundi wawili wabobezi wa utengenezaji vioo wakifika Tanzania kushiriki mafunzo na kubadilishana ujuzi.

Aliongeza kuwa wadau wa sekta ya ubunifu wameunga mkono mradi huo, wakiuona kama daraja muhimu la kuimarisha uhusiano wa watu kwa watu (people-to-people connection), wenye manufaa makubwa kijamii na kiuchumi.

Kwa ujumla, ushirikiano huo unaendelea kuleta matokeo chanya katika kukuza sanaa, ubunifu na kuimarisha mahusiano ya kimataifa kati ya Italia na Tanzania.













Na Janeth Raphael - MichuziTv

Rais Samia amesema Taifa litamkumbuka William Lukuvi kama kiongozi aliyegusa maisha ya wengi kwa moyo wake wa upendo, hekima, na kujitolea kwa dhati katika utumishi wa umma.

"Hayati Lukuvi atabaki katika kumbukumbu zetu si tu kwa nafasi alizoshika, bali kwa namna alivyoweza kujenga mahusiano mema na ya kudumu ndani ya jamii"

Pia Rais Samia amesema LUKUVI alikuwa kiongozi aliyesikiliza, aliyeshirikiana na makundi mbalimbali, na aliyethamini mchango wa kila mmoja katika kujenga taifa.

Katika kipindi hicho ambacho dunia inakumbwa na changamoto nyingi na mabadiliko yasiyotabirika, umuhimu wa kuwa na viongozi wenye uzoefu mpana na waliopitia ngazi mbalimbali za uongozi hauwezi kupuuzwa

"Tulimuhitaji sana ndugu Lukuvi leo—zaidi hata kuliko jana—ili kuendelea kutoa mwongozo na busara katika nyakati hizi ngumu"

Aida Rais Samia amesema Maisha na utumishi wa LUKUVI vinatufundisha somo muhimu sana: kwamba uongozi ni dhamana, si fursa ya kujinufaisha, n wajibu wa kuitumikia jamii kwa uaminifu, uwajibikaji, na moyo wa kujitolea bila kuchoka, Haya ndiyo maadili aliyoyaishi, na huu ndio urithi wake kwa taifa letu"

Hata hivyo Rais Samia amesema ni jukumu letu sasa kuuenzi na kuuendeleza urithi huo Tuige mfano wake kwa kuimarisha mshikamano, kuheshimiana, na kufanya kazi kwa bidii kwa manufaa ya wote, kwa kufanya hivyo, tutakuwa tumemuenzi kwa vitendo, na kuhakikisha kuwa mchango wake unaendelea kuzaa matunda kwa vizazi vijavyo.














 Na Joseph Mahumi, WF


Serikali ya Tanzania imeendelea kung’ara katika jukwaa la kimataifa baada ya kuibuka mshindi wa jumla wa mwaka katika Tuzo za Usimamizi wa Deni la Umma za Jumuiya ya Madola na tuzo ya Ofisi Bora Kanda ya Afrika kupitia Idara ya Usimamizi wa Deni la Serikali, Wizara ya Fedha (Debt Management Division), ambazo zilitangazwa tarehe 26 Machi 2026 wakati wa Mkutano wa Jukwaa la Jumuiya ya Madola kuhusu Usimamizi wa Deni la Umma, uliofanyika jijini London, nchini Uingereza.

Ushindi huo mkubwa unatokana na juhudi za Serikali katika kuimarisha mifumo ya usimamizi wa deni la umma, ikiwemo kuunganisha vyema mifumo ya kifedha ya Serikali na kuboresha upatikanaji wa rasilimali fedha kwa ajili ya maendeleo, ambapo Jopo huru la wataalamu lililochambua mawasilisho kutoka nchi mbalimbali za Jumuiya ya Madola lilizingatia vigezo vya ubunifu, uimara na uendelevu katika kutoa tuzo hizo.

Akifungua hafla ya utoaji tuzo hizo, Naibu Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola, Bw. Tanmaya Lal, alisisitiza umuhimu wa nchi wanachama kuendelea kubuni mbinu madhubuti za kusimamia deni la umma ili kulinda uchumi dhidi ya misukosuko ya kifedha duniani.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu Mwandamizi wa Idara ya Uchumi, Maendeleo, Biashara na Uwekezaji wa Sekretarieti ya Jumuiya ya Madola, Bi. Ruth Kattumuri, aliipongeza Tanzania kwa mageuzi makubwa iliyoyafanya katika kuimarisha usimamizi wa deni la umma.

Alieleza kuwa mafanikio hayo ni kielelezo cha dhamira ya dhati ya nchi katika kujenga uchumi imara na unaostahimili mishtuko ya kiuchumi.

Aidha, Bi. Kattumuri, alisema kuwa Sekretarieti ya Jumuiya ya Madola itaendelea kuisaidia Tanzania katika juhudi zake za kuboresha sera na mifumo ya usimamizi wa deni, sambamba na utekelezaji wa maazimio ya Kikao cha 72 cha Kundi la Mawaziri wa Jumuiya ya Madola.

Mkutano huo wa Jukwaa la Jumuiya ya Madola uliofanyika kwa muda wa wiki moja uliwakutanisha wataalamu wa usimamizi wa deni kutoka nchi wanachama wa Jumuiya ya Madola kwa lengo la kubadilishana uzoefu, kujifunza na kujadili mbinu bora za kukopa, kusimamia na kulipa deni la umma, na umeandaliwa ikiwa ni sehemu ya Maadhimisho ya Mwaka wa Jumuiya ya Madola wa Deni Imara, Bunifu na Endelevu, ambapo Tanzania imejitokeza kama kinara na mfano wa kuigwa barani Afrika na katika Jumuiya nzima ya Madola.
Kamishna Msaidizi Idara ya Usimamizi wa Deni la Serikali, Wizara ya Fedha, Bw. Omary Khama (Katikati) akiwa ameshika tuzo mbili ambazo Tanzania imepata kwa kuibuka Mshindi wa jumla wa mwaka katika Tuzo za Usimamizi wa Deni la Umma za Jumuiya ya Madola na Tuzo ya Ofisi bora Kanda ya Afrika kupitia Idara ya Usimamizi wa Deni la Serikali, Wizara ya Fedha (Debt Management Division), ambazo zilitangazwa tarehe 26 Machi 2026 wakati wa Mkutano wa Jukwaa la Jumuiya ya Madola kuhusu Usimamizi wa Deni la Umma, uliofanyika jijini London, nchini Uingereza. Wengine katika picha ni Naibu Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola, Bw. Tanmaya Lal (kushoto) na  Mkurugenzi Mkuu Mwandamizi wa Idara ya Uchumi, Maendeleo, Biashara na Uwekezaji wa Sekretarieti ya Jumuiya hiyo, Bi. Ruth Kattumuri.
Kamishna Msaidizi Idara ya Usimamizi wa Deni la Serikali, Wizara ya Fedha, Bw. Omary Khama, akionesha tuzo mbili ambazo Tanzania imepata kwa kuibuka Mshindi wa jumla wa mwaka katika Tuzo za Usimamizi wa Deni la Umma za Jumuiya ya Madola na Tuzo ya Ofisi bora Kanda ya Afrika kupitia Idara ya Usimamizi wa Deni la Serikali, Wizara ya Fedha (Debt Management Division), ambazo zilitangazwa tarehe 26 Machi 2026 wakati wa Mkutano wa Jukwaa la Jumuiya ya Madola kuhusu Usimamizi wa Deni la Umma, uliofanyika jijini London, nchini Uingereza.
Kamishna Msaidizi Idara ya Usimamizi wa Deni la Serikali, Wizara ya Fedha, Bw. Omary Khama (Katikati) Aakiwa ameshika tuzo mbili ambazo Tanzania imepata kwa kuibuka Mshindi wa jumla wa mwaka katika Tuzo za Usimamizi wa Deni la Umma za Jumuiya ya Madola na Tuzo ya Ofisi Bora Kanda ya Afrika kupitia Idara ya Usimamizi wa Deni la Serikali, Wizara ya Fedha (Debt Management Division), ambazo zilitangazwa tarehe 26 Machi 2026 wakati wa Mkutano wa Jukwaa la Jumuiya ya Madola kuhusu Usimamizi wa Deni la Umma, uliofanyika jijini London, nchini Uingereza. Wengine katika picha ni washindi wenngine wa tuzo hizo kutoka nchi ya Barbados ambayo iliibuka mshindi wa Msimamizi bora wa deni katika ukanda wa nchi za Caribbean na Sri Lanka Msimamizi bora wa deni katika ukanda wa nchi za Asia.


Top News