Na Victor Masangu, Pwani

Vijana wapatao kumi kutoka baadhi ya mikoa mbali mbali wamefanikiwa kutinga katika kinyang'anyiro cha shindano la Vijana uchumi Challenge kwa mwaka wa 2026 ambalo kilele chake kinatarajiwa kufanyika Julai 6 mwaka huu katika ukumbi Mikutano wa Julius Nyerere International Convention Centre (JNICC), jijini Dar es Salaam.

Hayo yamebainishwa na Katibu Mkuu Ofisi ya Rais – Maendeleo ya Vijana, Jenifa Omolo ambaye alikuwa mgeni rasmi wakati wa halfa ya kufunga kambi rasmi ya vijana wapatao 100 ambao walikuwa wameweka kambi ya siku nne katika shule yaa uongozi wa Mwalimu Julias Nyerere iliyopo Kibaha Mkoa wa Pwani.

Katibu Oomolo amesema kwamba kambi hiyo ilikuwa na vijana wapatao 100 kutoka mikoa mbali mbali ya Tanzania bara na visiwani ambapo wameweza kufanyiwa usahili na kufanyiwa mchujo kutoka kwa majaji mahiri wapatao saba ambaao waliweza kuzingatia vigezo mbali mbali katika kufanya maamuzi na kuangalia mawazo ambayo yaliwasilishwa na vijana hao.

"Nimefaarijika sana kuwa mgeni rasmi katika kufunga kambi hii rasmi ya vijana wapatao 100 na wametoka sehemu mbali mbali na vijana hao wameweza kufanyiwa mchujo naa kubakia vijana 100 kati ya 100 ambao walikuwa kambi na kwamba watakwenda sasa katika fainali ambayo itafanyika katika ukumbi Mikutano wa Julius Nyerere International Convention Centre (JNICC), jijini Dar es Salaam,"amebaisha Omolo.

Kadhalika ameongeza kwamba mshindi wa kwanza katika shindano hilo la Vijana Uchumi Challenge atajinyakulia kitita cha kiasi cha shilingi milioni 50, ambapo mshindi wa pili atajisshindia shilingi elfu 30 na mshindi wa tatu anaondoka naa kiasi cha shilingi milioni 20 huku washindi wengine watapata kifuta jasho.

Amesema kuwa Serikali ya awamu ya sita itaendelea kuwapa sapoti kubwa na ushirikiano katika kuwawezesha vijana wote 100 waliofika hatua ya kambi ili kuhakikisha mawazo yao yanageuzwa kuwa miradi yenye tija.

Alifafanua Vijana Uchumi Challenge si shindano pekee, bali ni jukwaa la kuibua fikra za vijana, kulea ubunifu, kujenga ujasiri na kuthibitisha kuwa vijana wana nafasi kubwa ya kubuni suluhisho za changamoto za kiuchumi.

Omolo alibainisha kwa mujibu wa Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2022, Tanzania Bara ina vijana wenye umri wa miaka 15 hadi 35 wapatao milioni 20.6, sawa na asilimia 34.4 idadi inayoonesha kuwa taifa lina nguvu kazi kubwa ambayo ikitumia vipaji na kuendelezwa ipasavyo inaweza kuleta mageuzi makubwa ya kiuchumi.

Aliwataka vijana kutumia simu janja kama nyenzo ya kujiongezea kipato kwa kutumia teknolojia, pamoja na kunufaika na Mfuko wa Maendeleo ya Vijana na fursa nyingine zinazotolewa na Serikali.

Pia ametaja fursa nyingine kuwa ni mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na halmashauri kupitia mapato ya ndani, asilimia 30 ya zabuni zinazotengwa kwa makundi maalumu kupitia sheria ya manunuzi ya umma, pamoja na fursa zilizopo katika sekta za viwanda, uzalishaji na mnyororo wa thamani.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Kitaifa ya Vijana Uchumi Challenge, Joseph Malekela, alieleza mashindano hayo yalizinduliwa Aprili 10, 2026, na baada ya kupokea na kuchambua maombi 7,852, vijana 100 kutoka Tanzania Bara na Zanzibar, walichaguliwa kuingia kambini.

Akisoma risala kwa niaba ya washiriki, Raiyan Juma Amour kutoka Zanzibar aliiomba Serikali kufanya tathmini ya kimkakati ya mawazo yote 100 yaliyowasilishwa ili yaweze kutumika katika sekta mbalimbali na kuchangia kuleta mageuzi ya kiuchumi na kutatua changamoto zinazoikabili nchi.

Katika kilele cha fainali za shindano hilo la Vijana Uchumi challenge kwa mwaka 2026 ambalo linatarajiwa kufanyika Julai 6 mwaka katika ukumbi Mikutano wa Julius Nyerere International Convention Centre (JNICC), jijini Dar es Salaam ambapo mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan.





Na Farida Mangube, Morogoro

Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imewataka walimu nchini kuchangamkia fursa ya matumizi ya teknolojia ya Akili Unde (AI) katika ufundishaji na ujifunzaji ili kuongeza ufanisi wa kufundisha, kuboresha matokeo ya ujifunzaji na kuinua ubora wa elimu.

Akizungumza katika Mkutano Mkuu wa Chama cha Walimu wa Lugha ya Kiingereza Tanzania (TELTA) uliofanyika mkoani Morogoro, Mratibu wa EdTech kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dk. Alcardo Alex, alisema serikali imeweka kipaumbele katika matumizi ya teknolojia zinazoibukia, hususan Akili Unde, ili kuendana na mabadiliko ya kidijitali na kuimarisha sekta ya elimu.

Alisema wizara imeandaa miongozo ya matumizi ya Akili Unde katika ngazi zote za elimu, kuanzia elimu ya awali hadi vyuo vikuu, kwa lengo la kurahisisha ufundishaji na ujifunzaji, huku ikiendelea kuwajengea walimu uwezo wa kutumia teknolojia hiyo kwa ufanisi.

Aidha, alisema serikali imekamilisha madarasa janja 210 ambayo tayari yameanza kutumika, na inaendelea na mpango wa kuyasambaza katika maeneo mbalimbali nchini ili kuongeza matumizi ya teknolojia katika shule na taasisi za elimu.

Kwa mujibu wa Dk. Alex, matumizi ya Akili Unde yatawawezesha walimu kuandaa vipindi vya masomo, kutunga na kusahihisha mitihani, kufuatilia maendeleo ya wanafunzi na kuboresha mbinu za ufundishaji.

"Ni muhimu walimu kujifunza na kutumia teknolojia ya Akili Unde kwani ni fursa ya kuongeza maarifa, kubadilishana uzoefu na kuboresha ubora wa elimu," alisema Dk. Alex.

Akizungumza Katika atika mkutano huo, Kaimu Mkuu wa Ubalozi wa Marekani nchini Tanzania, Jeanne Clark, alisema walimu wa Tanzania wenye umahiri wa lugha ya Kiingereza na Kiswahili wana fursa ya kufundisha Kiswahili nchini Marekani iwapo wataendelea kuimarisha ujuzi wao wa lugha na kuendana na mabadiliko ya teknolojia.

Alisema mahitaji ya walimu wenye uwezo wa kutumia teknolojia za kisasa katika ufundishaji yanaongezeka duniani, hivyo ni muhimu walimu wa Tanzania kujiendeleza ili kunufaika na fursa za kimataifa.

Kwa upande wake, Mratibu wa TELTA, Dk. Ayoub Msuya, alisema matumizi ya Akili Unde yatawasaidia walimu kuandaa masomo kwa ubora zaidi, kuboresha mbinu za kufundishia na kuwasaidia wanafunzi kuelewa lugha ya Kiingereza kwa urahisi.

Naye Mkuu wa Idara ya Taaluma za Lugha katika Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine (SUA), Dk. Onesimo Nyinodi, alisema idara hiyo imepewa jukumu la kuratibu mafunzo ya matumizi ya Akili Unde kwa walimu wa lugha ya Kiingereza nchini.

Alisema mafunzo hayo yanalenga kuwawezesha walimu kutumia teknolojia hiyo kwa ufanisi katika kuboresha ufundishaji na matokeo ya ujifunzaji.








Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mhe. Martin Shigela, ameiagiza Halmashauri ya Wilaya ya Bukombe kubuni na kutekeleza miradi mipya ya kuongeza mapato, badala ya kuendelea kutegemea mapato ya madini peke yake.

Ametoa maelekezo hayo wakati wa Kikao Maalum cha Baraza cha kusikiliza na kujadili Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali [CAG]kwa mwaka wa fedha unaoishia Juni 2026.

Halmashauri ya Bukombe imepongezwa kwa kufaulu kupata Hati Safi katika ukaguzi wa CAG. Hati hiyo ni alama ya juu zaidi inayothibitisha kuwa fedha za umma zimetumika kwa uwazi na kwa mujibu wa sheria.

Kwa mujibu wa ripoti ya CAG, jumla ya hoja 24 zilibuliwa kwa mwaka 2026. Kati yake, hoja 5 zimeshatekelezwa na hoja 19 zinaendelea kutekelezwa

Mkuu wa Mkoa amewataka Madiwani kuacha tabia ya "kutengeneza hoja" ili zijibiwe, na badala yake kuzuia mapungufu kabla hayajatokea ili kuitunza taswira ya Serikali.

Halmashauri hiyo imefanikiwa kukusanya Shilingi Bilioni 5 za mapato ya ndani, sawa na asilimia 136.3 ya lengo. Hatua hiyo imeipatia sifa Halmashauri hiyo kutoka kwa Katibu Tawala wa Mkoa, Bw. Mohammed Gombat.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Bukombe, Mhe. Erick Kagoma, kwa niaba ya Madiwani, amesema amepokea na atatekeleza maelekezo ya kupunguza idadi ya hoja zinazoibuliwa na CAG katika miaka ijayo.








Wafanyabiashara wadogo na wa kati nchini wamepata fursa mpya ya kuongeza mtaji na kufanya malipo ya ndani na kimataifa, baada ya Benki ya NMB kwa kushirikiana na Mastercard kuzindua NMB SME World Business Credit Card jijini Arusha.

Akizungumza katika uzinduzi huo, Afisa Mkuu wa Wateja Binafsi na Biashara wa NMB, Filbert Mponzi, alisema kadi hiyo inatoa mkopo wa hadi Sh50 milioni, kulingana na uwezo wa mteja, pamoja na kipindi cha hadi siku 53 bila riba endapo deni litalipwa ndani ya muda huo. Huduma hiyo itawawezesha wafanyabiashara kuongeza bidhaa, kulipa wasambazaji kwa wakati na kukabiliana na changamoto za muda mfupi za mtaji.

Mbali na huduma ya mkopo, kadi hiyo inaweza kutumika kupitia mtandao wa Mastercard duniani na ina manufaa yanayojumuisha bima ya matibabu ya safari ya hadi dola 100,000, bima ya mizigo, huduma za VIP Lounge katika zaidi ya viwanja vya ndege 400 na punguzo katika hoteli na huduma mbalimbali.

Mkurugenzi wa Mastercard anayesimamia biashara za SME Afrika Mashariki na Visiwa vya Bahari ya Hindi, Imelda Ngunzu, alisema kadi hiyo itasaidia biashara kupata mtaji kwa wakati na kufanya malipo kwa usalama. NMB pia itaendelea kuwekeza katika huduma za QR, PayByLink na mashine za POS ili kuboresha ukusanyaji wa mapato na ukuaji wa biashara katika uchumi wa kidijitali.

 Afisa Mkuu wa Wateja Binafsi na Biashara, Filbert Mponzi (katikati), Mkurugenzi wa Mastercard anayesimamia biashara Afrika Mashariki, Imelda Ngunzu, na Meneja wa NMB Kanda ya Kaskazini, Baraka Ladislaus, wakizindua rasmi kadi maalumu ya NMB SME World Business Credit Card jijini Arusha. 





Na Mwandishi Wetu
WAFUGAJI wa kuku nchini wamehimizwa kutumia chakula bora cha mifugo ili kuongeza uzalishaji, kuboresha afya ya kuku na kuongeza faida ya biashara zao, huku vijana wakitakiwa kuchangamkia fursa za ufugaji wa kuku kama njia ya kujiajiri na kujikwamua kiuchumi.

Wito huo unakuja sambamba na upanuzi wa huduma za kampuni ya Ekama Animal Feeds ambayo imefungua rasmi tawi jipya la Gongolamboto, Dar es Salaam, litakaloanza kutoa huduma kuanzia Julai 1, 2026 kwa lengo la kuwasogezea wafugaji bidhaa na huduma za kitaalamu.

Kupitia tawi hilo jipya lililopo eneo la Mombasa-Gongolamboto, wafugaji watapata huduma za ushauri wa kitaalamu kutoka kwa madaktari wa mifugo bila malipo pamoja na huduma za usafiri bure, hatua inayolenga kupunguza gharama na kuwawezesha kupata huduma kwa urahisi.

Akizungumza na Wadau wa sekta ya mifugo,Meneja mauzo kutoka kampuni ya Ekama Animal Feeds Irene Temba amesema matumizi ya chakula bora ni msingi wa mafanikio katika ufugaji wa kuku kwani huchangia kuku kukua kwa haraka, kuongeza uzalishaji wa mayai na kupunguza magonjwa yanayoweza kuathiri biashara ya mfugaji.

Aidha, amesema kuwa vijana wengi wana nafasi kubwa ya kufanikiwa kupitia ufugaji wa kuku kutokana na ongezeko la mahitaji ya nyama na mayai nchini, hivyo wanapaswa kutumia fursa hiyo kwa kuanzisha miradi ya kisasa yenye kuzingatia matumizi ya lishe bora kwa mifugo.

Imeelezwa kuwa sekta ya ufugaji inaweza kuwa chanzo kikubwa cha ajira na kipato kwa vijana ikiwa watawekeza katika elimu ya ufugaji, matumizi ya teknolojia na bidhaa zenye ubora zinazowezesha kupata mavuno yenye tija.

Ekama Animal Feeds imeendelea kusambaza chakula cha kuku katika maeneo mbalimbali ikiwemo Bagamoyo, Kimara Suka, Zanzibar, Kongowe na sasa Gongolamboto, hatua inayoongeza upatikanaji wa bidhaa zake kwa wafugaji wa maeneo mbalimbali.

Ufunguzi wa tawi hilo jipya unatarajiwa kuimarisha huduma kwa wafugaji wa Dar es Salaam na maeneo ya jirani, huku ukiwa chachu ya kuhamasisha vijana wengi zaidi kuingia kwenye ufugaji wa kuku kama biashara yenye uwezo wa kuchangia ukuaji wa uchumi wa mtu binafsi na Taifa kwa ujumla.
WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali itaendelea kutekeleza miradi ya maendeleo iliyoahidiwa katika Mkoa wa Singida, ikiwemo barabara, reli ya kisasa (SGR), uwanja wa ndege pamoja na miradi ya maji, afya na elimu kwa lengo la kuchochea maendeleo ya wananchi na kukuza uchumi wa Taifa.

Ametoa kauli hiyo leo (Jumamosi, Juni 27, 2026) alipohutubia mkutano wa hadhara uliofanyika katika Uwanja wa Maonesho wa Mandewa, wilayani Ikungi, mkoani Singida, ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya kikazi mkoani humo.

Waziri Mkuu amesema Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amemtuma kuwahakikishia wananchi wa Mkoa wa Singida kuwa miradi yote ya maendeleo iliyoahidiwa itaendelea kutekelezwa hatua kwa hatua kwa kuzingatia vipaumbele vya Serikali.

"Mheshimiwa Rais amenituma niwahakikishie kwamba mambo ambayo wabunge wenu wamekuwa wakiyasema na ambayo aliwaahidi wananchi wa Singida yatakwenda kutekelezwa," amesema.

Amesema Serikali itaendelea kutekeleza miradi ya barabara ikiwemo Sabasaba–Sepuka–Ndago–Kizaga, Njia Panda–Makiungu–Mungaa–Misughaa–Ndago, Mkiwa–Itigi–Rungwa–Makongorosi, Iguguno–Nduguti–Sibiti, pamoja na Singida–Ilongero–Haydom, hatua zitakazorahisisha usafirishaji, biashara na kufungua fursa zaidi za kiuchumi katika Mkoa wa Singida na maeneo jirani.

Aidha, amesema Serikali itaendelea na utekelezaji wa reli ya kisasa (SGR) itakayofika Singida pamoja na ujenzi wa uwanja wa ndege wa kisasa utakaohudumia ndege za ukubwa mbalimbali na kuongeza fursa za uwekezaji na biashara.

Waziri Mkuu amesema kuchelewa kwa baadhi ya miradi kulitokana na uamuzi wa Serikali kuelekeza rasilimali katika kukamilisha miradi ya kimkakati ikiwemo Mradi wa Kufua Umeme wa Julius Nyerere, Reli ya Kisasa (SGR) na Daraja la Kigongo–Busisi, ambayo sasa imeanza kutoa manufaa makubwa kwa Taifa.

"Tulifanya uamuzi wa kufunga mkanda ili tukamilishe miradi ya kimkakati. Leo Tanzania ina ziada ya umeme na miradi hiyo imeendelea kutoa manufaa makubwa kwa wananchi na uchumi wa Taifa," amesema.

Amesema Serikali itaendelea kuboresha huduma za maji, afya, elimu na miundombinu mingine ya kijamii sambamba na utekelezaji wa miradi hiyo ili kuongeza ustawi wa wananchi wa Mkoa wa Singida na Taifa kwa ujumla.






Na MWANDISHI WETU, Dar es Salaam


Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM - Bara) Ndg Stephen Wasira, amewataka Watanzania kuhifadhi na kuishi kulingana na urithi wa Mwalimu Julius Nyerere.

Akizungumza katika mahojiano maalumu, na ujumbe kutoka Serikali ya Angola, leo Juni 27, 2026. Wasira amemuelezea Mwalimu Nyerere kuwa kiongozi wa kipekee ambaye aliwaunganisha wananchi, alitawala kwa uadilifu mkubwa, na kuondoka madarakani bila kujilimbikizia mali.

Wasira alisema mojawapo ya sifa kuu za Mwalimu Nyerere ni uwezo wake wa kuwahamasisha Watanzania kushiriki kikamilifu katika masuala muhimu ya kitaifa badala ya kuwa watazamaji ukiwemo ulinzi wa taifa lao.

“Aliwashirikisha watu wote. Akieleza sababu ya vita, akawaambia ‘vita hii ni yetu sote.’ kila Mtu alipoona kiongozi wake anamweleza wazi hivi ndivyo ilivyotokea, hivi ndivyo tulivyoamua…basi mtu alishiriki moja kwa moja,”alisema Wasira akirejea Vita ya Kagera.

Kuhusu urithi halisi wa Nyerere, Wasira alitaja mambo mawili makuu ambayo yanapaswa kulindwa kwa umakini.

“Jambo moja tunalolikumbuka na tunalojaribu kulihifadhi kati ya aliyotuachia ni Uhuru. Pili ni Umoja. Kwa sababu Umoja hapa ni kitu tunachojivunia sana, nchi isiyo na ukabila, ambapo watu wa makabila na dini tofauti wanaishi pamoja kwa amani.” Amesema.

Alisema sehemu iliyogusa zaidi katika mazungumzo hayo yalikuwa maelezo ya Wasira kuhusu maisha ya Mwalimu Nyerere baada ya kung’atuka madarakani.

“Vizazi vijavyo vitamkumbuka Mwalimu Nyerere kama mtu aliyepigania uhuru wa nchi yake. Aliongoza nchi yake kwa miaka 24 kama Rais, na akaondoka madarakani akaenda kijijini. Akarudi kuwa mkulima mdogo. Hakuwa na pesa. Hakuwa na akaunti benki nje wala ndani ya nchi. Ni mtu wa kipekee sana,” alisema.

Aidha, alisema Mwalimu Nyerere aliamini kwamba uhuru wa Tanganyika hauwezi kuwa matunda zaidi pasipo nchi zingine za bara hilo kuwa huru.

"Mwalimu Nyerere aliamini kwamba uhuru wa Tanganyika bila uhuru wa Afrika kwamba usingekamilika mpaka nchi zote za Afrika ziwe huru.

“Alitoa mchango mkubwa wa ukombozi hasa kwa nchi za Kusini mwa Afrika, na mwisho aliamini katika umoja wa Afrika jambo ambalo hadi anaondoka duniani hakuweza kulikamilisha,” alieleza.






Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro imeanza utekelezaji wa mpango maalum wa kuboresha eneo la Endoro ili litumike kama sehemu ya utalii tiba kwa watalii pamoja na shughuli nyingine zinazohitaji utulivu.

Kamishna wa Uhifadhi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro Abdul-Razaq Badru akiwa na Wakurugenzi wa Bodi katika eneo hilo lenye Maporomoko ya Maji (Water Falls), Mapango ya Tembo, Msitu, Wanyama wakubwa na maarufu kwa utalii wa kutembea (Walking Safaris)

Ameeleza kuwa kupitia fedha za Mfuko wa Maendeleo ya Utalii (TDL) eneo la Endoro linaboreshwa kwa ujenzi wa miundombinu ya kisasa ya Utalii  ili yatumike kama sehemu za utalii tiba, utafiti, utalii wa kutembea, mapumziko binafsi na kuondoa msongo wa mawazo.

“Endoro ni eneo lenye utulivu, lina kivutio cha Mapango ya Tembo na maporomoko ya maji yenye urefu wa mita 40, mamlaka imeamua kuboresha miundombinu yake ili mgeni akifika hapa na hasira aweze kupata utulivu na kurudi katika hali yake ya kawaida”,alisema kamishna Badru.

Makamu Mwenyekiti wa bodi hiyo Dkt. Harieth Mtae amepongeza jitihada hizo na kusema zitatoa fursa ya kuongezeka kwa  idadi ya watalii wanaotembelea kivutio hicho kilichopo hifadhi ya Ngorongoro.

Wakurugenzi wa bodi hiyo pia wamekagua geti la kisasa la kuingilia ndani ya hifadhi linalofanya kazi katika mfumo wa kisasa pamoja na minara ya mawasiliano ndani ya hifadhi inayolenga kuboresha huduma kwa watalii. 


















Top News