Na Oscar  Assenga Tanga

Jukwaa la Wanawake na Kodi limefanyika leo Jijini Tanga huku ikielezwa ni hatua muhimu inayodhihirisha dhamira ya kuendeleza usawa wa kijinsia na kukuza uchumi shirikishi nchini.

Akizungumza wakati akifungua Jukwaa hilo Meneja wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Tanga, CPA Castro John, alisema ni dhamira ya dhati ya kujenga mfumo wa kodi unaoshirikisha makundi yote ya jamii, hususan wanawake ambao ni nguzo muhimu ya uchumi wa Taifa.

Alisema takwimu zinaonesha wanawake wanachangia kwa kiwango kikubwa katika shughuli mbalimbali za kiuchumi zikiwemo biashara ndogondogo, kilimo, huduma, viwanda vidogo pamoja na biashara za kati na kubwa.

Kwa mujibu wa takwimu za mwaka 2024/2025, wanawake nchini, wakiwemo wa Mkoa wa Tanga, wanakadiriwa kushiriki katika nguvu kazi kwa asilimia 80, huku wakimiliki asilimia 54 ya biashara ndogo, za kati na kubwa.

“Bila ushiriki wa wanawake, juhudi za kuongeza wigo wa walipa kodi na kuongeza mapato ya ndani haziwezi kufikia malengo yaliyokusudiwa,” alisema CPA Castro John.

Alifafanua kuwa TRA imeanzisha Jukwaa hilo maalumu kwa lengo la kutoa elimu sahihi ya kodi, kusikiliza changamoto za wanawake wafanyabiashara, kujenga ushirikiano wa karibu pamoja na kuhamasisha ulipaji wa kodi kwa hiari na kwa wakati.

Aidha, alisema TRA imejikita katika kuboresha huduma kwa kuzingatia ushirikishwaji, uwazi, weledi na urahisi wa upatikanaji wa huduma. Aliongeza kuwa elimu ya kodi na mahusiano bora ni msingi muhimu wa kuongeza utii wa kodi.

Kupitia jukwaa hilo, wanawake watapata nafasi ya kupata ushauri kuhusu masuala ya kodi, kujifunza fursa mbalimbali pamoja na kuelewa wajibu wao wa kikodi.

“Tunataka mwanamke ajisikie salama, aheshimiwe na ashiriki kikamilifu katika mfumo wa kodi bila hofu wala kikwazo chochote,” alisema.

CPA Castro John alisisitiza kuwa kodi ndiyo injini ya maendeleo ya Taifa kwani mapato yake yanagharamia huduma muhimu kama elimu, afya, barabara, maji safi na miradi mingine ya kimkakati.

“Kila mwanamke anayelipa kodi anakuwa mshirika wa moja kwa moja wa Serikali katika kujenga Tanzania yenye uchumi imara na huduma bora kwa wananchi wake,” aliongeza.

Pia aliwataka wanawake kutumia jukwaa hilo kujifunza, kuuliza maswali na kuwa mabalozi wa utamaduni wa kulipa kodi katika jamii zao.

Aidha, aliwataka wadau wa sekta mbalimbali pamoja na taasisi za kifedha kuendelea kushirikiana na TRA katika kuwawezesha wanawake kukuza biashara zao kwa kuzingatia misingi ya kikodi.

Kwa upande mwingine, aliwahimiza wanawake wafanyabiashara kujisajili katika mfumo wa kodi na kutekeleza wajibu wao kwa hiari na kwa wakati.

“Kulipa kodi si wajibu wa kisheria tu, bali ni mchango wa moja kwa moja katika kujenga Taifa. Wanawake wakisimama kiuchumi, familia na jamii vinaimarika,” alisema.

Katika hatua nyingine, alisisitiza umuhimu wa kutumia mipaka rasmi ya biashara kwa wafanyabiashara wanaovuka mipaka kupitia maeneo ya Horohoro na Pangani, huku akiwataka kuachana na biashara za magendo na matumizi ya njia zisizo rasmi.

Naye Naibu Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Wafanyabiashara nchini, JW Ismail Masound, alisema jukwaa hilo lina umuhimu mkubwa kutokana na malengo ya Dira ya Taifa ya mwaka 2050 ambapo sekta binafsi inatarajiwa kuwa mhimili mkubwa wa ukuaji wa uchumi.

Alisema majukwaa hayo yanasaidia kuwawezesha wanawake na wafanyabiashara kufikia malengo ya maendeleo ya Taifa kwa kuongeza ushiriki wao katika shughuli za kiuchumi.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Jukwaa la Wanawake Mkoa wa Tanga (TWCC), Aziza Ramadhani, alisema jukwaa hilo litawasaidia wanawake kuelewa umuhimu wa kulipa kodi katika kukuza uchumi wa Mkoa wa Tanga na Taifa kwa ujumla.

“Hivyo ni wajibu wetu kuhakikisha Mkoa wa Tanga unalipa kodi kutokana na umuhimu wake kwa maendeleo ya jamii,” alisema.

Aliongeza kuwa jukumu la jukwaa hilo ni kuwaunganisha wanawake wa Mkoa wa Tanga ili kuwapa nafasi ya kujifunza, kushirikiana na kupata fursa mbalimbali za kiuchumi ndani na nje ya mkoa huo.

Aidha, alisema wamekuwa wakitoa mafunzo mbalimbali ikiwemo kuanzisha mashamba darasa kwa vijana wa kiume na wa kike, huku akiwakaribisha wanawake wajasiriamali kushiriki katika shughuli za maendeleo zinazochangia ukuaji wa uchumi wa Mkoa wa Tanga na Taifa kwa ujumla.




Shirika la Umeme Tanzania TANESCO Mkoa wa Ruvuma limezindua ofisi ndogo ya TANESCO katika kijiji cha Nyerere, kata ya Mtina wilayani Tunduru, kwa lengo la kusogeza huduma za umeme karibu na wananchi wa eneo hilo.

Akizungumza katika uzinduzi huo, Mkuu wa Wilaya ya Tunduru, Denis Masanja, amemwagiza Meneja wa TANESCO pamoja na timu yake kuhakikisha wanaitumia ofisi hiyo kufanya kazi usiku na mchana ili kutatua changamoto za umeme katika kata ya Mtina na maeneo ya jirani.

Kwa upande wake, Kaimu Meneja wa TANESCO Mkoa wa Ruvuma, Boniface Malibe, amesema kuwa lengo la kuanzishwa kwa ofisi hiyo ni kusogeza huduma zote muhimu karibu na wananchi wa kata hiyo, ambao hapo awali walilazimika kufuata huduma mjini umbali wa zaidi ya kilometa 40.

Amesema uwepo wa ofisi hiyo utasaidia kupunguza ucheleweshaji wa kushughulikia hitilafu mbalimbali za umeme na kuongeza ufanisi wa huduma kwa wananchi.

Nao wananchi wa kata ya Mtina wameeleza kuwa eneo hilo limekuwa likikumbwa na changamoto za umeme kwa muda mrefu, lakini wameonesha matumaini makubwa kufuatia uzinduzi wa ofisi hiyo ndogo ya TANESCO, wakiamini itarahisisha upatikanaji wa huduma na utatuzi wa changamoto zinazojitokeza.







Mbunge wa Jimbo la Mbinga vijijini na Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Judith Kapinga amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan, inaendelea kuleta mageuzi makubwa katika sekta za elimu na afya hasa maeneo ya Jimbo hilo kupitia utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo.

Akizungumza katika Kijiji cha Mapera, Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga Mkoani Ruvuma, wakati wa uwekaji wa jiwe la msingi kwenye mradi wa vyumba vinne vya madarasa uliofanywa na Kiongozi wa Mbio za Mwenge Kitaifa.

Amesema Serikali imeendelea kutoa ruzuku kwa shule za msingi na sekondari jambo linalowezesha wanafunzi kupata elimu bila kulipa ada, huku ikiendelea kuboresha mazingira ya kujifunzia kupitia ujenzi wa madarasa na miundombinu mingine muhimu.

“Serikali ya Rais Samia imeonyesha dhamira ya kweli ya kuwekeza katika elimu na maendeleo ya wananchi, hii ndiyo sababu miradi ya elimu inaendelea kutekelezwa kwa kasi katika maeneo mbalimbali.”

Aidha, amesema Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga imeendelea kuunga mkono juhudi hizo kwa kutumia sehemu ya mapato yake ya ndani kugharamia ujenzi wa madarasa, ameeleza kuwa halmashauri hiyo hukusanya zaidi ya shilingi bilioni 13 kwa mwaka na hutenga kiasi cha fedha kwaajili ya ujenzi wa vyumba vya madarasa.

Pamoja na hilo, amewataka wazazi na walezi kuhakikisha wanawapeleka watoto shule ili waweze kunufaika na fursa za elimu zinazotolewa na Serikali, pamoja na kuwasimamia watoto wao waende shule kupata elimu.

Katika hatua nyingine, Mhe. Kapinga amemshukuru Kiongozi wa Mbio za Mwenge kwa kukubali kuweka jiwe la msingi katika mradi wa ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Mbinga Vijijini wenye thamani ya shilingi bilioni 3.7.

Amesema Serikali imeahidi kuongeza shilingi bilioni moja katika mwaka wa fedha ujao kwa ajili ya kuendelea kuboresha huduma na mazingira ya hospitali hiyo.

Akiwa Kata ya Maguu, Mhe. Kapinga amewaomba wananchi wa Mbinga Vijijini kuendelea kuwa na imani na Serikali ya awamu ya sita, kutokana na maboresho yanayoendelea kufanyika katika sekta ya kilimo kwa kuhakikisha wakulima wanapata pembejeo kwa wakati, hususan kwa zao la kahawa licha ya changamoto zilizopo, wananchi wanaendelea kuwa wanufaika wakubwa.

Kwa upande wake Wazo Michael Mwang’onda kiongozi wa mbio za mwenge kitaifa mwaka 2026, amewapongeza viongozi wa Halmashauri pamoja na Mbunge wa Jimbo hilo kwa usimamizi mzuri wa miradi ya maendeleo, amehimiza upendo na mshikamano kama Taifa chini ya kauli mbiu ya mwaka huu isemayo “Tanzania ni yetu sote tushirikiane kwa pamoja kuleta Maendeleo”.

Na Pamela Mollel,Arusha 

Serikali ya Tanzania imesema itaendelea kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi na nchi ya Urusi kupitia sekta mbalimbali ikiwemo kilimo, uchimbaji na uchakataji wa madini pamoja na uwekezaji katika viwanda vikubwa vya dawa vitakavyosaidia kuboresha huduma za afya na kuongeza ajira kwa wananchi

Kauli hiyo imetolewa jijini Arusha na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo wakati akizungumza katika jukwaa la biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na Urusi lililowakutanisha viongozi, wawekezaji na wafanyabiashara kutoka mataifa hayo mawili

“Tanzania itaendelea kufungua milango ya uwekezaji na kushirikiana na mataifa mbalimbali ili kuhakikisha sekta muhimu za uzalishaji zinakuwa na mchango mkubwa katika kukuza uchumi wa nchi,” amesema Profesa Kitila Mkumbo

Amesema ushirikiano huo utafungua fursa mpya za maendeleo, kuongeza thamani ya mazao na madini pamoja na kusaidia upatikanaji wa teknolojia na huduma muhimu kwa wananchi

Kwa upande wake, Waziri wa Maendeleo ya Uchumi wa Shirikisho la Urusi, Maksim Reshetnikov amesema Tanzania ni moja ya nchi zenye fursa kubwa za uwekezaji kutokana na mazingira mazuri ya biashara yanayoendelea kuimarishwa

“Urusi ipo tayari kuendelea kushirikiana na Tanzania katika sekta mbalimbali za uchumi kwa manufaa ya mataifa yote mawili,” amesema Maksim Reshetnikov

Jukwaa hilo la biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na Urusi limewakutanisha wafanyabiashara, wawekezaji pamoja na viongozi mbalimbali kwa lengo la kutafuta fursa za uwekezaji, kujadili changamoto za biashara na kupanua masoko kati ya nchi hizo mbili.








Na Pamela Mollel,Arusha 

Maonesho ya kimataifa ya utalii ya KARIBU-KILIFAIR 2026 yanatarajiwa kuifungua Arusha kama kitovu cha sekta ya utalii Afrika Mashariki, huku zaidi ya waoneshaji 550 kutoka mataifa 14 pamoja na mawakala na waendeshaji wa safari zaidi ya 1,000 kutoka nchi zaidi ya 40 wakitarajiwa kushiriki katika tukio hilo litakalofanyika kuanzia Juni 4 hadi 7, 2026 katika viwanja vya Magereza Kisongo mkoani Arusha

Maonesho hayo ambayo yameendelea kujijengea hadhi kama jukwaa kubwa zaidi la utalii katika ukanda wa Afrika Mashariki, yanatarajiwa kuvutia zaidi ya wageni na wadau wa utalii 15,000 kutoka sehemu mbalimbali duniani, hatua inayozidi kuthibitisha nafasi ya KARIBU-KILIFAIR kama lango muhimu la biashara na uwekezaji wa utalii barani Afrika

Wakizungumza na waandishi wa habari jijini Arusha, Wakurugenzi wa Kilifair Promotions, Tom Kunkler na Dominic Shoo, wamesema maonesho hayo yalizaliwa baada ya kuunganishwa kwa maonesho mawili makubwa ya utalii nchini Tanzania ambayo ni KARIBU Fair chini ya TATO pamoja na KILIFAIR ya Kilifair Promotions, muungano ambao umeifanya Tanzania kuwa mwenyeji wa moja ya maonesho yenye ushawishi mkubwa zaidi wa utalii Kusini mwa Jangwa la Sahara

Kwa mujibu wa waandaaji hao, tofauti na miaka iliyopita, maonesho ya mwaka 2026 yatafanyika kwa siku nne kamili huku yakipanuliwa hadi kufikia eneo lenye ukubwa wa mita za mraba 47,000, hatua inayolenga kutoa nafasi zaidi kwa washiriki, wawekezaji na wadau wa sekta hiyo

Tom Kunkler amesema dhamira yao imeendelea kujengwa katika misingi ya ubunifu, viwango vya kimataifa na mpangilio wa kisasa wa maonesho, huku mwaka huu wakianzisha maeneo mapya ikiwemo “Pan Africa Pavilion” chini ya kampeni ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya “Visit East Africa – Feel the Vibe”, inayolenga kuitangaza Afrika Mashariki kama kitovu cha kipekee cha utalii duniani

Aidha, amesema kaulimbiu ya maonesho hayo ya “Where Business Meets Wildlife” imeendelea kuonesha namna Tanzania ilivyo na nafasi adhimu katika utalii wa mikutano na biashara, ambapo fursa za uwekezaji na biashara zinaenda sambamba na vivutio vya asili, wanyamapori na utamaduni wa kipekee

Waandaaji hao pia wameishukuru Serikali ya Tanzania chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan kwa mchango wake katika kukuza sekta ya utalii pamoja na Wizara ya Maliasili na Utalii, Waziri Dkt. Ashatu Kijaji, Bodi ya Utalii Tanzania (TTB), TANAPA na wadau mbalimbali wanaoendelea kushirikiana kuhakikisha maonesho hayo yanakuwa na mafanikio makubwa zaidi kila mwaka

Kwa upande wake Mkuu wa Kanda wa Yas Makao Makuu Dar es Salaam, Robert Sanyagi, amesema ushiriki wa kampuni hiyo katika maonesho ya KARIBU-KILIFAIR 2026 ni sehemu ya mkakati wa kuendelea kusogeza huduma za kidijitali karibu na wadau wa sekta ya utalii pamoja na wananchi kwa ujumla. Amesema maonesho hayo yanatoa fursa muhimu kwa kampuni hiyo kukutana moja kwa moja na wateja wake, kusikiliza mahitaji yao na kuwaonesha teknolojia mpya zinazolenga kuboresha mawasiliano nchini

Sanyagi ameongeza kuwa Yas imejipanga kuonesha uwezo wa teknolojia ya 5G ambayo imeanza kupanuliwa katika maeneo mbalimbali ya Tanzania, hususan ukanda wa Kaskazini ambako shughuli nyingi za utalii hufanyika. Amesema teknolojia hiyo itasaidia kuongeza kasi ya intaneti, kurahisisha mawasiliano ya biashara na kuboresha huduma kwa watalii na wawekezaji wanaoshiriki katika maonesho hayo makubwa ya kimataifa.

KARIBU-KILIFAIR imeendelea kuwa dirisha muhimu la kuitangaza Tanzania kimataifa kupitia vivutio vyake vya asili na utamaduni vinavyotajwa kuwa miongoni mwa bora duniani. Baadhi ya vivutio hivyo ni pamoja na Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, Bonde la Ngorongoro pamoja na Mlima Kilimanjaro ambao ni mlima mrefu zaidi barani Afrika. Vivutio vingine ni pamoja na Hifadhi ya Taifa ya Mikumi, Hifadhi ya Taifa ya Ruaha na Pori la Akiba la Selous, sambamba na fukwe za kuvutia za Dar es Salaam zinazozidi kuwavutia watalii kutoka mataifa mbalimbali duniani.







▪️Wajadili mipango endelevu ya ujenzi wa miundombinu

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amekutana na kufanya kikao kazi na wabunge wa mikoa ya Mwanza, Mara na Simiyu pamoja na viongozi kutoka Wizara ya Uchukuzi, Wizara ya Ujenzi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI pamoja na Wizara ya Fedha.

Lengo la kikao hicho lilikuwa ni kujadili maendeleo ya miradi ya kimkakati ya miundombinu katika mikoa hiyo hususan ukamilishaji wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwanza pamoja na viwanja vya ndege vya Serengeti na Musoma.

Kikao hicho kilifanyika katika Ukumbi wa Spika, Bungeni jijini Dodoma, leo Ijumaa Mei 15, 2026, pia kilihudhuriwa na Mkuu wa Mkoa wa Mwanza pamoja na wakuu wa taasisi za usafirishaji na miundombinu ikiwemo reli, barabara na viwanja vya ndege pamoja na wataalamu mbalimbali kutoka Serikalini.









KATIKA maadhimisho ya Siku ya Familia Duniani, wito umetolewa kwa familia za Tanzania kuzingatia uzazi wa mpango kama njia muhimu ya kujenga familia imara, kukuza uchumi na kuhakikisha watoto wanapata malezi bora yatakayowawezesha kufikia ndoto zao.

Imeelezwa kuwa familia ndiyo taasisi ya msingi katika ujenzi wa taifa, uchumi na maendeleo ya nchi yoyote duniani, lakini changamoto ya ongezeko kubwa la watu imeendelea kuwa kikwazo kwa familia nyingi kumudu gharama za malezi, elimu na afya kwa watoto.

Takwimu zinaonesha kuwa Tanzania ina ongezeko la watu linalozidi asilimia tatu kwa mwaka, kiwango ambacho ni kikubwa kuliko wastani wa Bara la Afrika wa asilimia mbili na wastani wa dunia wa asilimia moja. Hali hiyo imeelezwa kuongeza mzigo wa utoaji wa huduma za kijamii huku taifa likikabiliwa na changamoto ya kujenga rasilimali watu yenye ubora.

Kwa mujibu wa tathmini ya maendeleo ya uchumi, Tanzania kwa sasa ipo nafasi ya 81 kwa ukubwa wa uchumi duniani na ya 165 kwa pato la mtu mmoja, huku ikiwa nafasi ya 20 kwa idadi ya watu duniani. Makadirio yanaonesha kuwa ifikapo mwaka 2050, idadi ya watu inaweza kufikia takribani milioni 137, jambo litakalohitaji uwekezaji mkubwa katika elimu, afya na ajira ili kuhakikisha wananchi wanapata maisha bora.

Aidha, imeelezwa kuwa nchi kama China zilipata mafanikio ya haraka ya kiuchumi kutokana na sera za kudhibiti ongezeko la watu, huku India ikiwa na changamoto ya pato la mtu mmoja licha ya kuwa miongoni mwa mataifa yenye uchumi mkubwa duniani. Hali hiyo imeelezwa kuwa somo kwa Tanzania katika kupanga ukuaji wa uchumi unaokwenda sambamba na ukuaji wa watu.

Wadau wa maendeleo wameeleza kuwa ili Tanzania ifikie malengo ya maendeleo ya muda mrefu, kuna haja ya kujenga familia zenye watoto wachache lakini wenye afya, maadili, elimu na maarifa yatakayowawezesha kushindana katika soko la dunia. Pia imesisitizwa kuwa uwekezaji katika sekta za elimu na afya hauwezi kutegemea kodi na mikopo pekee, bali unahitaji ushirikiano wa sekta ya umma na binafsi (PPP) ili kuhakikisha kizazi kijacho kinakuwa nguvu kazi yenye tija kwa taifa.

 


Na Mwandishi wetu- MBEYA

Mkurugenzi msaidizi wa Kituo cha Taifa cha Operesheni na Mawasiliano  ya Dharura kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Bi. Jane Kikunya amewataka Wajumbe wa Timu  ya kukabiliana na Dharura na Uendeshaji  wa Kitio  cha Operesheni  na Mawasiliano  ya Dharura ya  Mkoa wa  Mbeya kufanya kazi kwa ushirikiano, mshikamano na mawasiliano ya karibu ili kutekeleza wajibu wao kwa weledi na ufanisi unaotakiwa.

Mkurugenzi huyo, ameyasema hayo wakati akifungua mafunzo ya siku tano yanayolenga kuziandaa timu za kukabiliana na Maafa za Mkoa huo.

Aidha, mafunzo hayo  ambayo yaliyoandaliwa na Ofisi ya Waziri Mkuu yanatolewa kwa Wajumbe wa Kamati ya Wataalamu ya Usimamizi  wa Maafa, Wajumbe wateule wa Timu ya kukabiliana na Dharura ya Mkoa na wataalamu wa Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura, Waratibu wa Maafa Mkoa na Halmashauri.

Vilevile, Bi. Jane amesema mafunzo hayo yatakuwa mhimili muhimu katika kuhakikisha Mkoa unajiandaa vyema ili kukabiliana na matukio ya dharura kwa haraka hivyo ni lazima timu lengwa ifanye kazi kwa mshikamano ili kuleta ufanisi unaohitajika.

Kwa upande wao  wanufaika wa mafunzo hayo wameishukuru Serikali kwa namna inavyofanya jitihada kuhakikisha wananchi wanaishi katika mazingira salama.

Hivyo, wameahidi kutumia elimu hiyo ya kukabiliana na maafa pindi yanapotokea kuokoa maisha ya watu, mali zao  na kurejesha hali.






Mwanandishi wetu, Morogoro.
WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais, Mhe. Mhandisi Hamad Masauni amesema Usimamizi na uhifadhi wa mazingira hauwezi kufanikiwa kwa kauli au sera peke yake, bali kwa vitendo vinavyoonekana katika ngazi zote ikiwemo shughuli za kupanda miti na kuitunza.

Amesema maono na Matarajio ya Dira 2050 ni makubwa na yanahitaji ubunifu mkubwa katika kufanya kazi ili kufikia matarajio hasa katika mikakati mahsusi ya hifadhi na ustahimilivu wa mabadiliko ya tabianchi.

Waziri Masauni ameyasema hayo Mei 15, 2026 wilayani Kilosa mkoani Morogoro kwenye zoezi la upandaji miti ili kuhakikisha mazingira yanabaki kuwa salama kutokana na uoto wa asili ikiwa moja shughuli zilizopangwa na Ofisi ya Makamu wa Rais kuelekea Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani itakayofanyika Juni 5 mwaka huu ambapo kitaifa itafanyika mkoani Dodoma.

Amesema Dira ya Taifa ya mwaka 2050 ina nguzo kuu tatu na miongoni mwa nguzo hizo ni suala zima la uhifadhi wa mazingira na utahimilivu wa mabadiliko ya tabianchi jambo ambalo kila mmoja anapaswa kulitazama kwa upana wake.

"Haya tunayoyaona hapa kama vile athari za mafuriko, hali ya hewa isiyotabilika inayosababisha ukame na madhara mengine mengi miongoni mwa sababu zake ni mabadiliko ya tabianchi, hivyo kama taifa ni lazima tutoe kipaumbele katika kuhakikisha athari za mabadiliko ya tabianchi tunazihimili," amesema Masuni.

Ameongeza kuwa mtu anaweza asione faida ya upandaji miti lakini ukweli ni kuwa miti hiyo inafaida kuwa katika suala zima la upandaji miti hasa kwa kizazi kichacho cha miaka 50 ijayo kwani ndiyo wenye Tanzania ya baadaye.

Aidha Waziri Masauni aliipongeza Wilaya ya Kilosa na mkoa mzima wa Morogoro kwa kuwahusisha wananafuzi wa shule za msingi na sekondari katika suala zima la upandaji miti na utunzaji mazingira.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Kilosa, Mhe. Shaka Hamdu Shaka kwa niaba ya Mkuu wa mkoa wa Morogoro alisema kuwa wilaya hiyo imejiwekea malengo ya kupanda miti milioni 1.5 na kwamba zoezi hilo limekuwa likifanyika kila mwaka kwa mfululizo wa miaka mitano.

Mhe. Shaka amesema kuwa wilaya yake mara kwa mara imekuwa ikikubwa na mafuriko na kwamba katika kukabiliana na hali hiyo, serikali imedhamilia kujenga mabawa ya maji katika maeneo ya mto Mkondoa ili kuweza kudhibiti mafuriko, hivyo zoezi la upandi miti hiyo kutasaidia kulinda na kufidhi bwawa hilo na hivyo kuchochea maendeleo mbalimbali ya kiuchumi.
Na Mwandishi wetu- MBEYA

Mkurugenzi msaidizi wa Kituo cha Taifa cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Bi. Jane Kikunya amewataka Wajumbe wa Timu ya kukabiliana na Dharura na Uendeshaji wa Kitio cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura ya Mkoa wa Mbeya kufanya kazi kwa ushirikiano, mshikamano na mawasiliano ya karibu ili kutekeleza wajibu wao kwa weledi na ufanisi unaotakiwa.


Mkurugenzi huyo, ameyasema hayo wakati akifungua mafunzo ya siku tano yanayolenga kuziandaa timu za kukabiliana na Maafa za Mkoa huo.

Aidha, mafunzo hayo ambayo yaliyoandaliwa na Ofisi ya Waziri Mkuu yanatolewa kwa Wajumbe wa Kamati ya Wataalamu ya Usimamizi wa Maafa, Wajumbe wateule wa Timu ya kukabiliana na Dharura ya Mkoa na wataalamu wa Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura, Waratibu wa Maafa Mkoa na Halmashauri.

Vilevile, Bi. Jane amesema mafunzo hayo yatakuwa mhimili muhimu katika kuhakikisha Mkoa unajiandaa vyema ili kukabiliana na matukio ya dharura kwa haraka hivyo ni lazima timu lengwa ifanye kazi kwa mshikamano ili kuleta ufanisi unaohitajika.
Kwa upande wao wanufaika wa mafunzo hayo wameishukuru Serikali kwa namna inavyofanya jitihada kuhakikisha wananchi wanaishi katika mazingira salama.

Top News