Dar es Salaam, Julai 3, 2026 

Serikali imekipongeza Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) kwa mafanikio makubwa ya kupanua huduma zake nchini, hatua iliyowezesha kuongeza fursa za mafunzo kwa watumishi wa umma na wananchi kupitia ongezeko la kampasi kutoka mbili hadi sita katika kipindi cha miaka 25 iliyopita.

Pongezi hizo zimetolewa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Ridhiwani Jakaya Kikwete, wakati wa kilele cha maadhimisho ya miaka 25 ya TPSC yaliyofanyika katika Julius Nyerere International Convention Centre.

"Katika kipindi cha miaka 25 iliyopita, Chuo hiki kimepitia hatua kubwa za maendeleo. Kutoka kampasi mbili wakati wa kuanzishwa kwake hadi kufikia kampasi sita leo; kutoka programu chache za mafunzo hadi kuwa taasisi inayotoa mafunzo ya muda mfupi, programu za muda mrefu, mafunzo kwa njia ya mtandao, tafiti tumizi na shauri za kitaalamu," alisema Kikwete.

Alisema maendeleo hayo yanaonesha dhamira ya TPSC ya kuhakikisha mafunzo ya utumishi wa umma yanawafikia Watanzania wengi zaidi na kukidhi mahitaji yanayoongezeka ya Serikali katika kujenga watumishi wenye ujuzi, weledi na maadili.

Mbali na kupanua mtandao wa kampasi, Kikwete alisema Chuo kimeongeza wigo wa programu zake za mafunzo kwa kuanzisha mafunzo ya muda mfupi, muda mrefu na mafunzo kwa njia ya mtandao, sambamba na kuimarisha tafiti tumizi na ushauri wa kitaalamu unaosaidia taasisi za umma kuboresha utendaji wake.

Alibainisha kuwa mafanikio hayo yameifanya TPSC kuwa moja ya taasisi muhimu za Serikali katika kuendeleza rasilimali watu na kuimarisha utoaji wa huduma kwa wananchi.

Kwa niaba ya Serikali, Kikwete aliwapongeza viongozi wote waliowahi kuongoza Chuo, wafanyakazi wa sasa na wa zamani, Bodi za Ushauri pamoja na wadau mbalimbali kwa mchango wao katika mafanikio hayo, akisema hatua iliyofikiwa ni matokeo ya maono ya uongozi, ushirikiano na uzalendo wa watumishi waliojitolea kuijenga TPSC kuwa taasisi yenye hadhi ya kitaifa na kikanda























 

Na Janeth Raphael MichuziTv 

Maonesho ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba) yameelezwa kuwa moja ya majukwaa makubwa yanayochochea ukuaji wa biashara, uwekezaji na ubunifu nchini, huku yakiiunganisha Tanzania na masoko ya kikanda pamoja na ya kimataifa.

Akizungumza katika ufunguzi rasmi Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam leo, Ijumaa Julai 3, 2026, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema maonesho hayo yameendelea kuwa nguzo muhimu ya maendeleo ya sekta ya biashara kwa kipindi cha nusu karne.

Rais Samia amesema Sabasaba imekuwa jukwaa linalowakutanisha wazalishaji, wafanyabiashara, wawekezaji na wanunuzi kutoka ndani na nje ya nchi, jambo ambalo limeongeza fursa za biashara na kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi.

Amebainisha kuwa mafanikio ya maonesho hayo yanaonekana kupitia wafanyabiashara wengi walioanza safari zao kwa mitaji midogo wakitumia Sabasaba kutangaza bidhaa na huduma zao, lakini sasa wamekua na kuwa miongoni mwa wafanyabiashara wakubwa wanaochangia kwa kiasi kikubwa ukuaji wa uchumi wa taifa.

Aidha, amesema maonesho hayo yameendelea kuwa chanzo cha manufaa kwa wakulima, wajasiriamali na wabunifu kwa kuwapatia nafasi ya kutafuta masoko mapya, kujifunza teknolojia na mbinu za kisasa za uzalishaji, pamoja na kupata washirika na mitaji ya kukuza shughuli zao za kiuchumi.

Kwa mujibu wa Rais Samia, Sabasaba imeendelea kuijengea Tanzania taswira nzuri kama kitovu cha biashara na uwekezaji katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kusini mwa Afrika, huku pia ikifungua milango ya masoko katika Bara la Afrika na sehemu nyingine duniani.

Ametoa wito kwa waandaaji wa maonesho hayo pamoja na wadau wa sekta binafsi kuendelea kubuni mbinu mpya zitakazoyawezesha Maonesho ya Sabasaba kufikia viwango vya kimataifa, ili yaendelee kuwa chachu ya ukuaji wa uchumi, ajira na maendeleo ya biashara nchini.









Na Mwandishi Wetu

Dar es Salaam. Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imeendelea kutumia Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara (Sabasaba) kutoa elimu kwa wananchi kuhusu majukumu yake, huduma mbalimbali na umuhimu wa ithibati katika kuimarisha taaluma ya uandishi wa habari nchini.

Hatua hiyo imejidhihirisha leo baada ya Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa JAB, Wakili Patrick Kipangula, kuungana na maafisa wa Bodi katika banda la JAB lililopo Kijiji cha Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, kutoa elimu kwa wananchi, kujibu maswali mbalimbali na kuzungumza na waandishi wa habari waliotembelea banda hilo.

Akizungumza katika maonesho hayo, Wakili Kipangula alisema JAB imejipanga kuhakikisha wananchi na wadau wa sekta ya habari wanapata uelewa sahihi kuhusu majukumu ya Bodi pamoja na huduma zinazotolewa kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari.

Alisema ushiriki wa JAB katika maonesho ya Sabasaba unalenga kusogeza huduma karibu na wananchi, kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa ithibati kwa waandishi wa habari na kuhamasisha uzingatiaji wa maadili, weledi na uwajibikaji katika taaluma ya uandishi wa habari.

Mbali na kutoa elimu, JAB inaendelea kutoa huduma mbalimbali katika banda lake ikiwemo usajili wa waandishi wa habari, utoaji wa vitambulisho vya ithibati kwa waliokidhi vigezo, marekebisho ya taarifa za usajili pamoja na ushauri kuhusu huduma zinazotolewa na Bodi.

JAB imewahimiza waandishi wa habari, wadau wa sekta hiyo na wananchi kwa ujumla kutumia fursa ya Maonesho ya Sabasaba kutembelea banda lake ili kupata huduma, elimu na ufafanuzi kuhusu shughuli zake, huku ikisisitiza kuwa ithibati ni nyenzo muhimu katika kujenga taaluma ya uandishi wa habari yenye weledi, uwajibikaji na kuaminika.

Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa SGA Tanzania, Oscar Mgaya akizungumza wakati wa hafla hiyo.

Naibu Kamishna wa Polisi (DCP) Ulrich Matei (kushoto) akikabidhi zawadi Kwa John Amon ambaye ni mmoja wa wastaafu wa SGA Tanzania.
Naibu Kamishna wa Polisi (DCP) Ulrich Matei (wa pili kushoto) akisaidiana na wanachama wa Club 20 wa SGA kukata keki wakati wa shughuli ya kuwaaga wafanyakazi waliostaafu na kuwatambua wafanyakazi walihudumia kampuni hiyo kwa zaidi ya miaka 20. 

JESHI la Polisi limetoa wito wa ushirikiano wa karibu kati ya polisi na makampuni binafsi ya ulinzi kwa lengo la kupunguza matukio ya uhalifu pamoja na kudumisha amani nchini.

Wito huo umetolewa hivi karibuni na Naibu Kamishna wa Jeshi la Polisi (DCP) Ulrich Matei wakati wa hafla maalum iliyoandaliwa na kampuni ya ulinzi ya SGA Tanzania iliyolenga kuwaaga watumishi wa kampuni hiyo waliosataafu na kuwatambua wafanyakazi walioitumikia kampuni hiyo Kwa zaidi ya miaka 20.

baada ya kutumikia kampuni hiyo kwa zaidi ya miaka 20 kupitia programu inayojulikana kama Club 20.

Hafla hiyo ilifanyikia katika Bustani ya Hekima jijini Dar es Salaam na kuhudhuriwa na wawakilishi mbalimbali kutoka Jeshi la Polisi, Baraza la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA), uongozi na wafanyakazi wa kampuni ya SGA pamoja na wageni wengine waalikwa.

Alisema kuwa sekta binafsi katika sekta ya ulinzi pia ina jukumu la kuhakikisha nchi inakuwa salama amapo alitoa wito kwa wastaafu walioagwa kuendelea kutoa michango na uzoefu wao ili amani iliyoko hapa nchini iendelee kutamalaki.

DCP Matei aliupongeza uongozi wa SGA kwa kuendelea kuthamini michango inayotolewa na wafanyakazi wake sambamba na kuhakikisha ustawi wa watumishi wa kampuni hiyo ikiwemo kuendelea kuwajengea uwezo.

”Makampuni mengi huwa hayazingatii maagizo yanayoelekeza makampuni binafsi ya ulinzi kuendelea kuwajengea mazingira mazuri ya kiutendaji watumishi wao kupitia mafunzo, uhakiki, usimamizi na maboresho ya mishahara; kwa SGA niwapongeze kwa kujitahidi kutekeleza maagizo haya, nyinyi ni mfano mzuri wa kuigwa na makampuni mengine”, alisema.

Aidha alitoa pongezi kwa uongozi wa kampuni hiyo kwa kuwa na utaratibu wa kuwapongeza wafanyakazi waliofanya kazi kwa zaidi ya miaka 20 na kuongeza kwamba kwa watumishi zaidi ya 95 kufanya kazi kwa zaidi ya miaka 20 ni jambo linalostahili kusherehekewa na kupongezwa.

Alitoa wito kwa makampuni yote ya ulinzi ya binafsi kuongeza ufanisi na kuwekeza zaidi katika teknolojia, mafunzo kwa watumishi wao, kufuata sheria na kuzingatia haki za binadamu ili kupunguza malalamiko wakati wa utoaji wa huduma.

DCP Matei aliahidi kuwa Jeshi la Polisi litaendelea kutoa ushirikiano wake wa dhati kwa makampuni binafsi jambo ambalo amesema ni muendelezo wa ushirikiano huo kwa miaka mingi iliyopita.

Akizungumza kwa niaba ya SGA Tanzania, Mkuu wa kitengo cha fedha cha kampuni hiyo Bw. Jonathan Geleta, aliushukuru uongozi wa Jeshi la Polisi kwa ushirikiano ambao jeshi hilo limetoa na linaendelea kutoa kwa makampuni binafsi ya ulinzi hapa nchini.

"Nichukue fursa hii kwa niaba ya uongozi wa SGA kuahidi kuwa kampuni yetu itaendelea kufuata miongozo na kanuni zote kama zinavyotolewa na Jeshi la Polisi ili kuhakikisha ufanisi katika kutoa huduma zetu ndani ya jamii”, alisema.

Aliwapongeza wastaafu kwa huduma yao bora waliyotoa wakati wakiitumikia kampuni hiyo, ambapo alitoa rai kwa wastaafu hao kuwa mabalozi wazuri wa kuhimiza amani wakati wakianza maisha mapya ndani ya jamii.

SGA Security ni kampuni ya kwanza ya ulinzi ya kibinafsi nchini Tanzania, iliyoanza kufanya shughuli zake rasmi hapa nchini miaka 42 iliyopita, ambapo kwa sasa inaajiri zaidi ya Watanzania 5,000 katika mtandao wake ulioenea hapa nchini.

Pamoja na huduma nyingine bora, kampuni hiyo pia inatoa huduma bora zaidi ya usafirishaji wa bidhaa zikiwemo zile zenye thamani kubwa kwa usalama wa hali ya juu na uhakika.

SGA pia inatoa huduma za ulinzi wa hali ya juu, huduma za dharura pamoja na vifaa vya usalama wa kielektroniki ambavyo husaidia kuhakikisha usalama wa wateja wake, ambapo kutokana na huduma hizo bora kampuni hiyo imepata tuzo mbalimbali za ndani na nje ya nchi.
Na. Mwandishi Wetu - Arusha

Tanzania ipo tayari kwa mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON 2027) ikiwa mwenyeji kwa kushirikiana na Kenya na Uganda ambapo maandalizi yamefikia hatua nzuri kwa kuzingatia viwango vya Shirikisho la Mpira wa Miguu Barani Afrika (CAF) vinavyotakiwa.

Akizungumza hii leo Julai 3, 2026 Jijini Arusha kwa niaba ya Mwenyekiti wa Kamati ya Kitaifa ya Makatibu Wakuu ya Maandalizi ya Michuano hiyo, Dkt. Jim Yonazi, Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii Dkt. Hassan Abbasi amesema Serikali imejipanga kikamilifu kuhakikisha michuano hiyo inafana kwa kuzingatia mipango na mikakati thabiti iliyopo.

Dkt. Abbasi ameiongoza Kamati hiyo iliyotembelea viwanja vitakavyotumika wakati wa michuano hiyo ikiwemo Kiwanja cha Mazoezi cha Mgambo, kiwanja cha mazoezi cha Engutoto, Kiwanja cha mazoezi Magereza, uwanja Mpya wa Arusha pamoja na ukaguzi wa barabara za mjini zinazosimamiwa na Wakala wa Barabara Tanzania-TANROADS pamoja na zinasosimamiwa na Wakala wa Barabara za mjini na vijijni -TARURA zitakazoingia na Kutoka Katika uwanja wa Arusha, kujionea maendeleo ya ukarabati na maboresho mbalimbali kuelekea michuano hiyo.

Aidha amesema kuwa, michuano hiyo itakuwa ya kihistoria kwa kukutanisha na kuvutia mamilioni ya watu barani Afrika na duniani kote, ambapo ni kwa mara ya kwanza mashindano hayo kuandaliwa kwa pamoja na Mataifa matatu ya Afrika Mashariki.

Aliongezea kuwa, Tanzania imejipanga kupokea Maelfu ya mashabiki, wachezaji, na viongozi wa soka wanatarajiwa kukusanyika na kuleta mwamko mkubwa kupitia Mashindano Makubwa ya Kombe la Mataifa Afrika (AFCON 2027).

"Ni wakati wetu sasa, kuipa nchi heshima yake kuelekea Michuano hiyo ya AFCON, kila mmoja akae tayari katika eneo lake na kujua kuwa anajukumu la kuifanikisha michuano hii na kwa viwango vya kimataifa," alisema Dkt. Abbasi.

Pia alisisistiza Wakandarasi kwenye miradi mbalimbali ya kuboresha miundombinu kuongeza kasi ili kumaliza kazi hizo kwa wakati bila kukwamisha maandalizi hayo.

Kwa upande wake Katibu Tawala wa Mkoa wa Arusha Dkt. Toba Nguvila amesema kuwa mkoa umeendelea na maandalizi yote muhimu ikiwemo ya ukarabati wa miundombinu itakayotumika, kuhakikisha upatikanaji wa huduma za maji, kuboresha maeneo ya utoaji wa huduma za kiafya ikiwemo hospitali, masuala ya mawasiliano, pamoja na umeme na kuhakikisha vinapatikana kwa ubora na viwango.

“Jiji linaimarisha miundombinu ya barabara, huku kukiwa na ujenzi na ukarabati wa hoteli za kutosha zitakazotoa huduma pamoja na uboreshwaji wa vituo vya afya vya kutolea huduma za afya ikiwemo hospitali ya Mount Meru, JKCI pamoja na NSK ambazo zitatoa huduma za kiafya kwa ubora na viwango,” alisema Dkt. Nguvila.










Top News