MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA) imefanya kikao na wadau wa michezo ya kubahatisha ikiwemo waendeshaji kutoka makampuni mbalimbali kwa lengo la kujadili masuala ya kodi.

Akimuwakilisha Kamishna wa Kodi za Ndani katika kikao hicho kilichofanyika leo tarehe 31 Julai, 2026 Serena Hotel jijini Dar es Salaam, Naibu Kamishna wa Walipakodi wa Kati Godwin Barongo amesema kuwa kodi itokanayo na michezo ya kubahatisha imeendelea kuwa na manufaa makubwa kwa Tanzania.

Barongo ameeleza kuwa kwa kipindi cha miaka tisa ya fedha kuanzia 2017/2018 ambapo kodi katika michezo hiyo ilianza kukusanywa hadi 2025/2026, mchango wa sekta hiyo umefikia takriban Shilingi Trilioni 1.463.

“Mchango huu mkubwa unaonesha umuhimu wa sekta hii katika kuchangia maendeleo ya taifa, na nawapongeza sana waendeshaji na wadau wote kwa ushirikiano mnaoendelea kuutoa,” amesema Barongo.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Oparesheni za Kimkakati wa Bodi ya Michezo ya Kubahatisha Tanzania Kabora Mboya ameipongeza TRA kwa kuendelea kuwakutanisha wadau wa sekta hiyo huku akisisitiza umuhimu wa ushirikiano endelevu katika kupata mafanikio.

Nao wadau wa sekta hiyo wamesema wapo tayari kuendelea kulipa kodi na kuiomba TRA na taasisi zingine za serikali kuendeleza utaratibu wa kukutana na wadau hao ili waweze kuimarisha ushirikiano na ufanisi wa utekelezaji wa wajibu wao.




📌 Shule ya Sekondari Nkololo yaachana na kuni pamoja na mkaa

Bariadi, Simiyu📍

Timu ya Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa imezindua rasmi mradi mkubwa wa ujenzi wa miundombinu ya nishati safi ya kupikia katika Shule ya Sekondari Nkololo, iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Bariadi Vijijini mkoani Simiyu.

Mradi huo, uliozinduliwa tarehe 30 Julai 2026, una lengo la kutokomeza kabisa matumizi ya kuni na mkaa katika taasisi zinazohudumia zaidi ya watu 100 kwa siku, kama sehemu ya kulinda mazingira na afya za Watu.

Akizungumza mara baada ya kukagua na kuzindua mradi huo, Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa, Bw. Wazo Michael Mwang’onda, aliipongeza Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kwa utekelezaji madhubuti wa mkakati huo wa serikali.

Bw. Mwang’onda alibainisha kuwa mradi huo utaleta tija kubwa kwa shule hiyo yenye jumla ya wanafunzi 606.

“Kupitia mradi huu, Serikali itapunguza kwa kiasi kikubwa matumizi ya kuni na mkaa wa kawaida. Hali hii itaboresha afya na usalama wa wanafunzi, walimu, pamoja na wapishi wanaotumia jiko hili kila siku,” alisema Kiongozi huyo.

Kwa upande wake, Mhandisi wa Miradi ya Nishati kutoka REA, Mha. Davidi Malima, alifafanua kuwa wakala huo umewekeza shilingi milioni 15 katika Shule ya Sekondari Nkololo. Fedha hizo zimefanikisha ununuzi wa majiko mawili makubwa yenye uwezo wa lita 200 kila mmoja, pamoja na usimamishaji wa tanki la gesi ya kupikia (LPG) lenye ukubwa wa tani moja.

Mha. Malima aliongeza kuwa mradi huo ni sehemu ya mpango mkubwa wa kitaifa unaolenga kuzifikia taasisi 453 katika mikoa yote nchini, ambapo jumla ya shilingi bilioni 25.8 zimetengwa.Mpango huu ni sehemu ya utekelezaji wa Mkakati wa Taifa wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia (2024–2034) wenye lengo la kuhakikisha asilimia 80 ya Watanzania wanatumia nishati safi ifikapo mwaka 2034.

Katika kufanikisha azma hiyo, kampuni ya Taifa Gas Limited ilishinda zabuni ya kusambaza na kufunga mifumo ya gesi ya LPG kwenye taasisi, huku kampuni ya Hanny G Investment ikikabidhiwa dhamana ya kusambaza majiko banifu na masufuria makubwa kote nchini.

Utekelezaji wa mradi huu unakuja wakati ambapo takwimu za mazingira nchini zikionyesha hali ya isiyoridhisha; ambapo Tanzania inapoteza zaidi ya hekta 370,000 hadi 470,000 za misitu kila mwaka. Sehemu kubwa ya uharibifu huu inasababishwa na uvunaji wa kuni na mkaa kwa ajili ya kupikia, huku zaidi ya asilimia 90 ya kaya na taasisi nchini zikiwa bado zinategemea nishati hiyo (Kuni na mkaa wa kawaida).

Mbali na uharibifu wa mazingira, matumizi ya kuni kwenye majiko yasiyo rasmi yanasababisha uchafuzi mkubwa wa hewa ndani ya nyumba na taasisi. Moshi wa kuni unaozalisha gesi hatari za ukaa (Carbon Monoxide) na chembechembe za moshi hubeba athari kubwa za kiafya, ikiwemo magonjwa ya mfumo wa upumuaji, matatizo ya macho, na hata vifo vya mapema kwa Watumiaji wa nishati hiyo.








Na Victor  Masangu,Bagamoyo 

Mwenyekiti wa Jumuiya ya  ya Wazazi Taifa Ndg. Fadhili Maganya amekemea vikali baadhi  viongozi wa CCM  wakiwemo madiwani na wabunge kuachana na vitendo vya kupanga safu hasa katika kuelekea kwenye uchaguzi wa mwaka 2027.

Hayo ameyabainisha  wakati wa ziara yake ya kikazi yenye lengo la kuweza kukiimarisha chama pamoja na jumuiya zake zote ikiwa samba samba na kuangalia uhai wa chama.

"Kitu kikubwa ninachowaomba viongozi,madiwani pamoja na wabunge  kuondokana kabisa na masuala ya kuamua kupanga safu kabla ya uchaguzi lkn kitu kikubwa wanaotaka kugombea ruksa kugombea nafasi mbali mbali,"amesema Mwenyekiti huyo.

Pia amefafanua kwamba mwakani ni kipindi cha uchaguzi hivyo hakusita kuwaasa wanachama wote kuanzia ngazi za mashina wasisite kujitokeza katika kugombea nafasi mbali mbali.

Kadhalika ameupongeza uongozi wa Wilaya ya Kisarawe kwa kuweza kusimamia vizuri utekelezaji wa ilani na ukusanyaji wa fedha za mapato ya ndani ambazo zimekwenda kutekeleza miradi ya maendeleo.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe Petro Magoti amesema kuwa hali ya  mwenendo  katika utekelezaji wa  miradi ya maendeleo inakwenda vizuri.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Mkuranga Nasri Ally amebainisha kuwa wameweza kufanikisha kukusanya mapato ya ndani kwa asilimi 113 na kuongeza  wana miradi 9 ya kimkakati ikiwemo mradi wa ujenzi wa ya kisasa.

Naye Mwenyekiti wa chama cha mapinduzi (CCM) Wilaya ya Kisarawe Halfan Sika amebainisha kwamba  wameweza kutekeleza ilani ya chama kwa vitendo ikiwa sambamba na kushirikiana na serikali katika miradi mbali mbali.

Mbunge wa Jimbo la Bagamoyo Kisarawe Selemani Jafo amempongeza Mwenyekiti wa  Taifa kwa kufanya ziara hiyo ya kikazi ambayo itaweza kuleta tija katika maendekeo kwa wananchi.

Mwenyekiti wa wazazi Mkoa wa Pwani Jackson  KItuka amewahimiza viongozi kuhakikisha wanapambana na winbi la baadhi ya matapeli wa ardhi kwani wamekuwa wakisababisha migogoro  ya ardhi. 

Akiwa Wilayani Mkuranga ameridhishwa na uchapa kazi wa Mkuu wa Wilaya ya Mkuranga kwa kuweza kusimamia vema utekelezaji wa miradi mbali mbali.

Mwenyekiti wa Jumuiya ya wazazi ya CCM Taifa ameendelea na ziara yake ya kikazi  katika Wilaya za Kisarawe pamoja na Wilaya ya mkuranga ambapo ametembelea miradi ya maendeleo ukiwemo Hospitali ya Kisarawe,daraja la Kisopwa,shule ya msingi sanze na chuo cha Veta mkuranga.






Na Janeth Raphael - MichuziTv

Benki ya Ushirika Tanzania (COOP Bank Tanzania) imefanya Mkutano Mkuu wake wa Pili tangu kuanzishwa kwake, ambapo viongozi na wanahisa walipokea taarifa ya mafanikio makubwa ya utendaji wa benki hiyo katika kipindi cha miaka miwili, yakionyesha ukuaji wa kasi katika sekta ya benki nchini.

Akizungumza wakati wa mkutano huo, Mkurugenzi Mtendaji wa COOP Bank Tanzania, Godfrey Ng'urah, amesema mkutano huo umekuwa fursa ya kutafakari safari ya mageuzi ya benki hiyo na hatua mbalimbali zilizofikiwa tangu kuanzishwa kwake.

Amesema mafanikio hayo yametokana na uongozi uliojikita katika mabadiliko, ambao umewezesha benki kuongeza kwa kiwango kikubwa rasilimali, wafanyakazi, matawi pamoja na ukubwa wa mizania ya benki ndani ya muda mfupi.

Ng'urah amesema viashiria vya utendaji vinaonesha kuwa COOP Bank ndiyo benki inayokua kwa kasi zaidi nchini kwa sasa, huku ikishuhudia ongezeko kubwa la wafanyakazi, upanuzi wa mtandao wa matawi na kuimarika kwa huduma zinazowafikia wateja katika maeneo mbalimbali.

Kwa upande wa utoaji wa mikopo, alisema benki imeendelea kuwawezesha wanachama wa vyama vya ushirika, wakulima, wafanyakazi, wafanyabiashara pamoja na taasisi mbalimbali za ushirika, ambapo kitabu cha mikopo kimeongezeka kutoka Sh bilioni 14 mwaka 2024 hadi kufikia Sh bilioni 102 mwaka 2025.

Aidha, amesema amana za wateja zimeongezeka kutoka Sh bilioni 15 hadi kufikia Sh bilioni 114 mwishoni mwa mwaka wa fedha uliopita, huku mtaji wa wanahisa ukikua kutoka Sh bilioni 27 hadi Sh bilioni 42, jambo linaloonyesha kuimarika kwa msingi wa kifedha wa benki hiyo.

Mkurugenzi huyo amebainisha kuwa COOP Bank imeendelea kupanua wigo wa bidhaa na huduma zake bunifu kwa kuanzisha akaunti nafuu zinazorahisisha uwekaji wa amana pamoja na kuwekeza katika miundombinu ya kidijitali inayowawezesha wateja kupata huduma kwa urahisi zaidi.

Ameongeza kuwa benki hiyo imezindua huduma ya COOP PESA, mfumo wa kisasa wa huduma za kibenki kupitia simu za mkononi unaowawezesha wateja kufanya miamala mbalimbali kwa urahisi, usalama na wakati wowote bila kulazimika kufika tawi.

Ng'urah amesema COOP Bank itaendelea kuwekeza katika ubunifu wa huduma za kifedha na teknolojia ili kuongeza ujumuishi wa kifedha, kuwafikia Watanzania wengi zaidi na kuchochea maendeleo ya sekta ya ushirika pamoja na uchumi wa nchi kwa ujumla.



Na Said Mwishehe,Michuzi TV

SERIKALI imeanzisha Chama cha Wahandisi wa Nishati (Association of Energy Engineers - AEE) Tanzania Chapter, hatua inayolenga kuimarisha ufanisi wa matumizi ya nishati, kupunguza upotevu wa umeme na kusaidia ukuaji endelevu wa sekta ya viwanda.

Chama hicho kilichoanzishwa kwa ushirikiano kati ya Serikali na Shirika la Umoja wa Mataifa la Maendeleo (UNDP), kitaongoza juhudi za kukabiliana na upotevu wa nishati unaokadiriwa kufikia asilimia 10 hadi 15, huku kikihamasisha matumizi bora ya nishati katika viwanda, taasisi na majengo ya biashara.

Akizungumza wakati wa uzinduzi jijini Dar es Salaam leo Julai 31,2026, Mkuu wa Kitengo cha Usimamizi wa Mazingira wa Wizara ya Nishati, Emilian Nyanda, alisema Tanzania imeweka sera na mikakati mbalimbali ya kuboresha ufanisi wa matumizi ya nishati, lakini mafanikio yake yanategemea uwepo wa wataalamu wenye ujuzi.

“Bila kuwa na wataalamu wa kutosha, itakuwa vigumu kufikia malengo ya taifa ya kuongeza ufanisi wa matumizi ya nishati,” alisema Nyanda.

Alisema utekelezaji wa Mpango Kazi wa Ufanisi wa Nishati umewezesha kuzalishwa kwa wakaguzi wa nishati 60 wenye ithibati, watakaosaidia kufuatilia matumizi ya nishati na kubaini maeneo yanayohitaji maboresho.

Nyanda alisema wataalamu hao watafanya ukaguzi katika viwanda, majengo ya biashara na taasisi za umma ili kubaini njia za kupunguza matumizi ya nishati bila kuathiri uzalishaji au utoaji wa huduma.

Alisema matumizi bora ya nishati yatasaidia kupunguza gharama za uzalishaji, hasa katika viwanda ambako umeme ni sehemu kubwa ya gharama za uendeshaji, hivyo kuongeza ushindani wa bidhaa zinazozalishwa nchini.

Aliongeza kuwa chama hicho kitatoa ushauri wa kitaalamu kwa Serikali kuhusu sera na mikakati ya nishati, huku kikihamasisha matumizi yenye uwajibikaji na kupunguza upotevu usio wa lazima.

Nyanda alisema kupunguza upotevu wa nishati kutapunguza pia shinikizo la uwekezaji katika miradi mipya ya umeme kwa kuhakikisha nishati inayozalishwa, ikiwemo kutoka Mradi wa Kufua Umeme wa Julius Nyerere, inatumika kwa ufanisi.

Meneja wa Maendeleo ya Vipaji wa UNDP, Veronica Sigalla, alisema AEE Tanzania Chapter inapaswa kuwa jumuishi kwa kutoa fursa kwa vijana, wanawake, wahandisi, mafundi, watafiti na wataalamu wa sekta ya nishati.

Alisema UNDP itaendelea kushirikiana na Wizara ya Nishati, Umoja wa Ulaya, Ubalozi wa Ireland na wadau wengine kuimarisha mfumo wa ufanisi wa matumizi ya nishati nchini.

Rais wa AEE Tanzania Chapter, Atupele Kilindu, alisema chama hicho kitakuwa jukwaa la wataalamu wa nishati kuimarisha ujuzi, kubadilishana maarifa, kukuza ubunifu na kuchangia utekelezaji wa malengo ya taifa katika sekta ya nishati.

“Kuanzishwa kwa AEE Tanzania Chapter kunaipa Tanzania jukwaa la kitaaluma litakalowawezesha wataalamu kuendelea kujifunza, kuendeleza ubunifu na kuunga mkono ajenda ya maendeleo endelevu ya nchi,” alisema Kilindu.

Alisema chama hicho kitaweka mkazo katika mafunzo ya kitaaluma, programu za uthibitishaji, utafiti, ubunifu, kulea wataalamu vijana na kuimarisha ushirikiano kati ya Serikali, taasisi za elimu, sekta binafsi na washirika wa maendeleo.
Mkuu wa Kitengo cha Usimamizi wa Mazingira wa Wizara ya Nishati, Emilian Nyanda (wapili kushoto) akizindua tawi la kwanza la Chama cha Wahandisi wa Nishati (Association of Energy Engineers - AEE) nchini, katika hafla iliyofanyoika leo jijini Dar es Salaam, watatu kulia ni Meneja wa Maendeleo ya Vipaji wa UNDP, Veronica Sigalla, na Rais wa AEE, Tupele Kilindu, katikati.






Na. Mtemi Sona

Dodoma. Mwenyekiti wa Ujenzi Sports Club, Arch. Ibrahim Chatila, amesema uongozi mpya umejipanga kuijenga timu hiyo kuwa ya kisasa, imara na yenye ushindani mkubwa katika mashindano yote itakayoshiriki.

Akizungumza kuhusu mikakati ya kuiboresha klabu hiyo iliyo chini ya Wizara ya Ujenzi, Chatila amesema lengo kuu ni kuunda kikosi chenye ubora wa hali ya juu kitakachokuwa na uwezo wa kushindana na timu mbalimbali nchini.

Amesema hatua za awali zitahusisha usajili wa wachezaji bora pamoja na kuimarisha benchi la ufundi kwa kuwashirikisha makocha wenye uwezo na sifa zinazohitajika ili kuongeza ushindani wa timu.

"Tunataka kuunda timu yenye wachezaji watakaoweza kuleta ushindi na ambao watazingatia weledi, nidhamu na taaluma katika kila mashindano tutakayoshiriki," amesema Chatila.

Mwenyekiti huyo ameongeza kuwa uongozi mpya uliochaguliwa umeazimia kuijenga upya Ujenzi Sports Club kwa misingi ya umoja, utawala bora na uwajibikaji kuanzia kwa viongozi, benchi la ufundi, wachezaji hadi wanachama.

Kwa mujibu wa Chatila, mafanikio ya timu hayatategemea ubora wa kikosi pekee, bali pia uimara wa mifumo ya uendeshaji wa klabu.

Mbali na masuala ya kiufundi, amesema uongozi wake umeweka mkazo katika kuimarisha uchumi wa klabu kwa kutafuta wadhamini na wadau mbalimbali watakaosaidia kuiendesha timu kwa kiwango cha kisasa.

"Lengo letu ni kuwa na klabu inayojitegemea kiuchumi, yenye uwezo wa kujiendesha na kushiriki mashindano kwa ushindani mkubwa," amesema.

Arch. Ibrahim Chatila ni Mbunifu Majengo kutoka Wakala wa Majengo Tanzania (TBA), ambayo ni moja ya taasisi zinazounda Ujenzi Sports Club. Pia ni kocha mwenye leseni ya CAF na amewahi kuwa mjumbe wa Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Singida kwa kipindi cha miaka minne.

Yeye ni miongoni mwa viongozi wapya waliochaguliwa hivi karibuni kuiongoza Ujenzi Sports Club, klabu inayoundwa na taasisi 10 zilizo chini ya Wizara ya Ujenzi.

Klabu hiyo hushiriki michezo mbalimbali ikiwemo mpira wa miguu, netiboli, riadha, kuvuta kamba na michezo mingine ya ushindani.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Alhaj. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amejumuika na waumini wa Dini ya Kiislamu katika Ibada ya Sala ya Ijumaa iliyosaliwa katika Msikiti wa Jamiu Zinjibar, Mkoa wa Mjini Magharibi.

Baada ya Sala ya Ijumaa, Rais Dkt. Mwinyi ameshiriki Sala ya Jeneza ya Marehemu Sheikh Abdullah Hamid Suleiman, aliyekuwa Khatibu katika misikiti mbalimbali Zanzibar, iliyosaliwa katika Msikiti wa Jamiu Zinjibar.

Marehemu Sheikh Abdullah Hamid Suleiman, amefariki dunia leo, tarehe 31 Julai 2026, na kuzikwa kijijini kwao, Muungoni, Makunduchi, Mkoa wa Kusini Unguja.








WAZIRI Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Nchemba, amesema Serikali chini ya uongozi wa Rais. Samia Suluhu Hassan inaendelea kuweka mazingira wezeshi ya kukuza vipaji vya vijana kupitia uwekezaji katika sekta ya michezo na ujenzi wa miundombinu ya kisasa.

Akizungumza usiku wa kuamkia leo, Julai 31 2026 wakati tamasha la mchezo wa Masumbwi “Knockout ya Mama Season 9” liliofanyika katika ukumbi wa The super Dome Masaki jijini Dar es Salaam, Waziri Mkuu amesisitiza mpango wa Serikali kujenga arena kubwa ya kisasa itakayokuwa kitovu cha matukio mbalimbali ya michezo na burudani nchini.

Amesema Rais Samia Suluhu Hassan anaendelea kuunga mkono juhudi za vijana na wadau wa michezo nchini, huku Serikali ikiendelea kushirikiana kwa karibu na sekta binafsi katika kuimarisha maendeleo ya michezo na kuibua vipaji.



Na Farida Mangube
Mtanzania Bi. Rehema Katuga kutoka Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria nchini (OCPD) ameibuka mshindi katika uchaguzi wa wajumbe wa Baraza la Uongozi na Usimamizi la Chama cha Wataalamu wa Uandishi wa Sheria wa Jumuiya ya Madola (Commonwealth Association of Legislative Counsel – CALC), na kuwa mmoja wa wawakilishi wawili wa Afrika katika baraza hilo.

Baraza hilo, lenye wawakilishi wawili kutoka kila bara, lina jukumu la kusimamia na kufanya maamuzi muhimu kuhusu uendeshaji wa chama hicho cha kitaaluma kinachowakutanisha wataalamu wa uandishi wa sheria kutoka nchi wanachama wa Jumuiya ya Madola.

Bi. Katuga aliibuka mshindi katika uchaguzi uliowahusisha wagombea wanne kutoka Afrika, wakiwemo wagombea wawili kutoka Afrika Kusini, mmoja kutoka Namibia na yeye akiwa mwakilishi pekee kutoka Tanzania. Ushindi huo umeiwezesha Tanzania kupata nafasi ya uwakilishi katika chombo hicho muhimu cha kitaaluma.

Akizungumzia umuhimu wa CALC, Bi. Katuga alisema chama hicho ni miongoni mwa vyama vya kitaaluma vinavyosimamiwa na Jumuiya ya Madola na kina jukumu la kuimarisha ushirikiano miongoni mwa wataalamu wa uandishi wa sheria katika nchi wanachama.

Alisema CALC inalenga kuimarisha uwezo wa wataalamu hao katika kuandaa sheria bora zinazotafsiri sera za Serikali na kuendana na mageuzi mbalimbali yanayohitajika katika nchi wanachama.

Aidha, chama hicho kinahamasisha ushirikiano katika mafunzo, kubadilishana uzoefu, programu za mafunzo kwa vitendo (attachments), matumizi ya teknolojia katika uandishi wa sheria pamoja na kuendeleza mbinu bora za taaluma hiyo.

“Lakini pia chama hiki kina Baraza la Uongozi linalojumuisha viongozi wakuu pamoja na wawakilishi kutoka mabara mbalimbali ambao ndio sisi tuliochaguliwa sasa. Kwa pamoja hushiriki katika kutoa mwelekeo na kufanya maamuzi kuhusu maendeleo ya taaluma ya uandishi wa sheria,” alisema Bi. Katuga.

Mwakilishi huyo wa Tanzania na Afrika alisema nafasi hiyo itamwezesha kuchangia kuimarisha ushirikiano wa wataalamu wa uandishi wa sheria nchini Tanzania na barani Afrika, kubadilishana maarifa na uzoefu na nchi nyingine za Jumuiya ya Madola, pamoja na kujifunza na kutumia mbinu bora za kisasa katika uandishi wa sheria.

Aidha, alisema anatarajia kushiriki kikamilifu katika kuunganisha wataalamu wa uandishi wa sheria barani Afrika, kukuza taaluma hiyo na kuchangia juhudi za kuboresha ubora wa sheria kupitia uandishi wenye weledi, uwazi na ufanisi.

Kwa Tanzania, uwakilishi huo unaongeza fursa ya kushiriki katika majadiliano ya kimataifa kuhusu maendeleo ya taaluma ya uandishi wa sheria na kunufaika na mafunzo, programu za kujengea uwezo wataalamu wa fani hiyo, pamoja na ubadilishanaji wa teknolojia na uzoefu. Hatua hiyo inatarajiwa kuchangia kuimarisha ubora wa mchakato wa uandaaji wa sheria nchini.

Matokeo ya uchaguzi huo yalitangazwa katika Mkutano Mkuu wa CALC uliofanyika tarehe 19 mwezi huu nchini Singapore.

Bayport Financial Services Tanzania imeadhimisha miaka 20 tangu kuanzishwa kwake kwa kutoa kompyuta 20 aina ya HP na mashine mbili za kuchapisha na kunakili (All-in-One Printers) zenye thamani ya jumla ya TZS milioni 100 kwa Idara ya Elimu ya Jimbo la Kibamba, ikiwa ni sehemu ya kuendeleza dhamira yake ya kusaidia sekta ya elimu na maendeleo ya taifa. 

Makabidhiano hayo yalifanyika rasmi katika hafla iliyofanyika katika Shule ya Msingi Anazaki, Kimara, na kuhudhuriwa na Mgeni Rasmi, Mheshimiwa Angellah Jasmine Kairuki, Mbunge wa Jimbo la Kibamba, pamoja na viongozi wa wilaya, maafisa wa elimu, wanahabari na wawakilishi wa Bayport.

 Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mkurugenzi Idara ya Mikopo Bayport Financial Services Tanzania, Amina Amani, alisema kuwa msaada huo ni sehemu ya juhudi za kampuni kuacha alama ya kudumu katika jamii wakati wa maadhimisho ya miaka 20 ya kuhudumia Watanzania.

 "Tulipotafakari namna bora ya kuadhimisha hatua hii muhimu, tulijiuliza ni kwa namna gani tunaweza kuacha urithi ambao utaendelea kuleta mabadiliko hata baada ya maadhimisho haya kuisha. Jibu lilikuwa wazi; tulitaka kufanya uwekezaji ambao utaendelea kuleta thamani kwa jamii na kuchangia safari ya maendeleo ya Tanzania kwa miaka mingi ijayo,"alisema Amani. 

Katika kipindi cha miaka 20 iliyopita, Bayport imehudumia zaidi ya Watanzania 430,439, wengi wao wakiwa watumishi wa umma, na kutoa mikopo yenye thamani ya zaidi ya TZS bilioni 529, iliyowasaidia wateja wake kutimiza malengo yao ya kifedha na maendeleo binafsi. 

Kompyuta na mashine za uchapishaji zilizotolewa zinatarajiwa kuimarisha mifumo ya usimamizi wa elimu kwa njia ya kidijitali katika Jimbo la Kibamba kwa kuongeza ufanisi wa kiutendaji, kuboresha utunzaji wa kumbukumbu na kuongeza upatikanaji wa teknolojia kwa maafisa wa elimu.

 "Kompyuta hizi ni zaidi ya vifaa vya teknolojia; ni fursa. Zitawawezesha maafisa wa elimu na walimu wanaojenga mustakabali wa taifa letu huku zikichangia kuboresha utoaji wa huduma kupitia mageuzi ya kidijitali," aliongeza Amani.

 Bayport imeeleza kuwa wakati Tanzania ikiendelea kutekeleza ajenda yake ya mageuzi ya kidijitali, upatikanaji wa teknolojia za kisasa ni muhimu katika kuboresha utoaji wa huduma za umma na kuandaa vizazi vijavyo kufanikiwa Katika uchumi wa kidijitali.

 Kampuni hiyo ilisisitiza kuwa mchango huo unaonesha dhamira yake ya kuwa taasisi inayowajibika kwa jamii na mshirika hai katika maendeleo ya taifa, mbali na jukumu lake la kutoa huduma za kifedha.

Bayport pia ilitoa shukrani kwa wateja wake, hususan watumishi wa umma wa Tanzania, ambao imani na ushirikiano wao vimewezesha ukuaji na mafanikio ya kampuni hiyo katika kipindi cha miongo miwili iliyopita.

 Mchango huu ni sehemu ya mpango wa Bayport wa Uwekezaji kwa Jamii (Corporate Social Investment) Katika maadhimisho ya miaka 20, unaolenga kuleta matokeo endelevu katika jamii zinazohudumiwa na kampuni hiyo.

 Akizungumza mara baada ya kupokea vifaa hivyo vya TEHAMA, Waziri Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Angellah Jasmine Kairuki ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Kibamba Mbunge wa Jimbo la Kibamba alisema kuwa msaada huo wa vifaa vya TEHAMA ni utekelezaji wa mkakati wa kuifanya Kibamba kuwa jimbo la kidijitali (Make Kibamba Digital) umeanza rasmi kwa kuimarisha matumizi ya teknolojia katika sekta ya elimu. 

Vifaa hivi vimekuja muda muafaka kwani vitarahisisha usimamizi wa elimu, mawasiliano kati ya idara mbalimbali, uratibu wa mitihani na utoaji wa huduma kwa walimu, wazazi na wanafunzi.

 “Tunaanza na idara za elimu, lakini huu ni mpango mpana wa kuifanya Kibamba kuwa jimbo la kidijitali. Tutaendelea kupeleka vifaa vya TEHAMA katika shule za sekondari, ofisi za kata na maeneo mengine ya huduma za umma kwa awamu,”amesema  Kairuki. 

Alibainisha kuwa tayari maandalizi yamekamilika kuzipatia shule za sekondari vifaa vya TEHAMA ikiwemo kompyuta, projectors na vifaa vingine vya kisasa, akisisitiza kuwa utekelezaji huo utafanyika hatua kwa hatua ndani ya kipindi cha miaka mitatu hadi minne. 

 Aidha, alitoa shukrani kwa Bayport Financial, pamoja na Idara ya Elimu ya Manispaa ya Ubungo kwa ushirikiano wao, akisema Bayport itaendelea kushirikiana na Serikali na jamii katika kutekeleza miradi yenye manufaa kwa wananchi.

Mkurugenzi Idara ya Mikopo Bayport Financial Services Tanzania, Amina Amani kulia akimkabidhi Waziri Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Angellah Jasmine Kairuki ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Kibamba, kumpyuta ya mezani kwa ajili ya Idara ya Elimu Jimbo la Kibamba. 

Bayport Financial Services Tanzania imeadhimisha miaka 20 tangu kuanzishwa kwake kwa kutoa kompyuta 20 aina ya HP na mashine mbili za kuchapisha na kunakili (All-in-One Printers) zenye thamani ya jumla ya TZS milioni 100 kwa Idara ya Elimu ya Jimbo la Kibamba, ikiwa ni sehemu ya kuendeleza dhamira yake ya kusaidia sekta ya elimu na maendeleo ya taifa. 


-Ni boti zinazotumia nusu saa Dar-Zanzibar ,Waziri Mkuu atoa maelekezo


Na Said Mwishehe,Michuzi TV

WAZIRI Mkuu Dk.Mwigulu Nchemba amesema Serikali itaendelea kuimarisha ulinzi na usalama katika Bahari na maziwa makuu ili kuhakikisha wanaofanya shughuli za kiuchumi katika maeneo hayo wanafanya kazi katika mazingira salama.

Akizungumza leo Julai 31,2026 katika viwanja vya bandari jijini Dar es Salaam wakati wa uzinduzi wa boti za doria katika bahari na maziwa makuu,Dkt. Mwigulu amesema Serikali imeweka ulinzi na usalama kuwa kipaumbele cha maendeleo ya taifa.

"Niwaletee salamu za Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye amenituma niwahakikishie kuwa Serikali itaendelea kuimarisha ulinzi na usalama katika maeneo ya maji ili wananchi wafanye shughuli zao kwa amani na usalama," amesema.

Ameongeza tayari Serikali imenunua vifaa vya kisasa vya uokoaji kwa Ziwa Victoria na sasa imeongeza uwezo wake kupitia uzinduzi wa boti mpya za doria zitakazosaidia kukabiliana na uhalifu na majanga katika bahari na maziwa.

Amefafanua hatua hiyo ni sehemu ya juhudi za Serikali kukabiliana na vitendo vya uhamiaji haramu, uharamia, usafirishaji wa dawa za kulevya, biashara haramu ya binadamu, uvuvi haramu, utoroshaji wa maliasili na unyang'anyi dhidi ya wavuvi.

“Mradi huu haujahusisha tu ununuzi wa boti za doria, bali pia umewezesha kuandaliwa kwa Mwongozo wa Kitaifa wa Kukabiliana na Uhalifu Baharini na Maziwani, kuanzishwa kwa Kituo cha Kitaifa cha Pamoja cha Operesheni, pamoja na kuwajengea uwezo wataalamu wa ndani kupitia mafunzo maalumu.”

Dk.Nchemba amesema usalama wa baharini ni muhimu kwa uchumi wa Tanzania kutokana na nafasi ya nchi kuwa lango la biashara kwa mataifa ya Afrika Mashariki na SADC.

"Kuimarika kwa usalama kutawapa wafanyabiashara na watumiaji wa Bandari ya Dar es Salaam uhakika zaidi wa kutumia lango letu la biashara," amesisitiza.

Aidha, ameagiza wizara na taasisi zote zinazohusika kutenga fedha za kutosha katika bajeti ya mwaka wa fedha 2027/28 kwa ajili ya uendeshaji, mafuta na matengenezo ya boti hizo ili zisikwame kutokana na ukosefu wa fedha.

Ametoa pia maelekezo kwa wasimamizi wa boti kuhakikisha zinafanyiwa matengenezo ya mara kwa mara na kutumika kwa kuzingatia miongozo ya kitaalamu.“Nazitaka wizara na taasisi zote zinazotakiwa kushiriki katika Kituo cha Kitaifa cha Pamoja cha Operesheni kupeleka wawakilishi wao ndani ya wiki mbili ili kituo hicho kianze kufanya kazi kikamilifu.

Pia ameishukuru Serikali ya Japan na Shirika la Umoja wa Mataifa la Maendeleo (UNDP), pamoja na washirika wengine wa maendeleo, kwa kufadhili mradi huo na kuahidi kuwa Serikali itaendelea kushirikiana nao katika kuimarisha usalama wa bahari na maendeleo ya uchumi wa buluu.

Kwa upande wake Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Profesa Palamagamba Kabudi amesema mradi huo umehusisha ununuzi wa boti mbili za doria, PB Sailfish II na PB Sailfish II, mafunzo kwa wataalamu wa kuzihudumia, pamoja na mradi ya kuwawezesha wakulima wa mwani katika Wilaya ya Mkinga, mkoani Tanga.

Ameongeza boti hizo zina uwezo wa kukimbia kwa kasi ya hadi knoti 50, sawa na takribani kilomita 92.6 kwa saa, hivyo kuongeza uwezo wa Serikali kufanya doria, kuzuia uhalifu baharini na kulinda rasilimali za bahari.”Spidi ya boti hizi zinatumia nusu saa kwenda Zanzibar na kurudi Dar.”

Awali akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Albert Chalamila, Mkuu wa Wilaya ya Ilala Edward Mpogolo amesema boti hizo ni utekelezaji wa Ilani ya CCM na juhudi za Serikali katika kuimarisha ulinzi na usalama pamoja na kukuza uchumi wa wananchi kupitia uchumi wa bluu.

“Boti hizi zitaongeza uwezo wa doria kuanzia Wilaya ya Kinondoni hadi Kigamboni, hivyo kuimarisha usalama wa wananchi na mali zao katika maeneo ya bahari.

Ameongeza boti hizo zitasaidia kudhibiti uvuvi haramu na kulinda rasilimali za bahari, hatua itakayowanufaisha wavuvi na wafanyabiashara wa samaki katika masoko ya Feri, Mbezi na Kigamboni.













Top News