Na Janeth Raphael -MichuziTv Singida 

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Nchemba, ameagiza kuchukuliwa hatua kali za kisheria dhidi ya watumishi wote wa umma watakaobainika kuhusika na ubadhirifu wa fedha za Serikali, akisisitiza kuwa tabia ya kuwahamisha badala ya kuwakamata imekuwa ikichangia kuendelea kwa vitendo vya wizi katika maeneo mbalimbali nchini.

Dkt. Mwigulu ametoa kauli hiyo leo Mei 31, 2026 wakati akizungumza na wananchi wa Itigi mkoani Singida, ambapo ameeleza kuwa Serikali haitavumilia watumishi wanaotumia nafasi zao vibaya kwa kuiba mali na fedha za umma zilizotokana na kodi za wananchi.

Amesema watumishi wanaobainika kufanya ubadhirifu hawapaswi kuhamishwa kutoka kituo kimoja cha kazi kwenda kingine kwani hatua hiyo haina tija, badala yake huwapa nafasi ya kuendelea kufanya vitendo hivyo katika maeneo mapya wanayopelekwa.

“Mwizi wala msimuhamishe. Mkishamhamisha anaenda kuiba na huko. Wale ambao walishahamishwa, kule walikopelekwa RPC wa huko awakamate,” alisema Waziri Mkuu huku akipigiwa makofi na wananchi waliohudhuria mkutano huo.

Katika hotuba yake, Dkt. Mwigulu alionesha kusikitishwa na baadhi ya watumishi wa umma wanaoshindwa kutambua dhamana waliyopewa na wananchi, akibainisha kuwa wengi wao wamepata elimu kwa gharama za Serikali kupitia kodi za Watanzania na baadaye kupewa nafasi za kazi ili kulitumikia taifa.

Amesema ni jambo la kushangaza kuona baadhi yao wakitumia nafasi hizo kwa manufaa binafsi badala ya kuwahudumia wananchi kwa uadilifu na uzalendo.

“Kuna watu hawamwogopi hata Mungu. Umesoma kwa kodi za Watanzania, umepata nafasi ya kuwatumikia wenzako, lakini unaamua kuwaibia. Wakati huo huo kuna vijana wengi wenye sifa wanaosubiri nafasi za ajira,” alisema.

Waziri Mkuu ameongeza kuwa Serikali inaendelea kupambana na vitendo vya rushwa, ubadhirifu na matumizi mabaya ya fedha za umma ili kuhakikisha rasilimali za nchi zinatumika kwa manufaa ya wananchi wote.

Aidha, alihoji mantiki ya kuendelea kuwahamisha watumishi wanaotuhumiwa kwa ubadhirifu huku Serikali ikibeba gharama za uhamisho wao, ikiwemo posho na nauli, jambo alilosema halina tija katika mapambano dhidi ya wizi wa mali za umma.

“Baada ya kuiba unataka tukuhamishe na tukulipie nauli ya kuhama. Hata hizo sheria tutazirejea. Mimi sichukii watu, lakini nachukia wizi,” alisisitiza.

Kauli ya Waziri Mkuu imekuja wakati Serikali ikiendelea kusisitiza uwajibikaji, uwazi na nidhamu katika utumishi wa umma, huku ikitaka fedha za wananchi zilindwe na kutumika ipasavyo kwa ajili ya kuharakisha maendeleo na kuboresha huduma za kijamii nchini.

Wakazi wa Itigi waliohudhuria mkutano huo walimpongeza Waziri Mkuu kwa msimamo wake dhidi ya ubadhirifu, wakieleza kuwa hatua kali dhidi ya wahusika zitasaidia kuongeza uwajibikaji na kuimarisha imani ya wananchi kwa taasisi za umma


Na Janeth Raphael MichuziTv Itigi - Singida

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Nchemba, ameielekeza Sekta ya Ardhi kujitathmini kwa kina na kuchukua hatua za haraka kurekebisha changamoto zinazoikabili, akieleza kuwa imeendelea kuwa chanzo kikubwa cha migogoro katika maeneo mbalimbali nchini.

Akizungumza na wananchi wa Itigi mkoani Singida leo Dkt. Mwigulu amesema kumekuwa na ongezeko la migogoro ya ardhi inayotokana na wizi, udanganyifu na uzembe wa baadhi ya watendaji, hali ambayo imekuwa ikisababisha wananchi kugombana na hata kuvuruga mshikamano wa kijamii.

Amesema migogoro hiyo imekuwa ikiwakosesha wananchi haki zao za msingi na kuathiri maendeleo ya jamii, huku baadhi ya wananchi wakijikuta wakipoteza ardhi zao kutokana na mifumo isiyo na ufanisi pamoja na vitendo vya rushwa vinavyohusishwa na baadhi ya watumishi wasio waadilifu.

Waziri Mkuu amesisitiza kuwa sekta hiyo inapaswa kufanya maboresho makubwa yatakayorejesha imani ya wananchi kwa kuhakikisha haki inatendeka kwa kila mwenye madai halali ya ardhi na kwamba serikali haitavumilia watendaji watakaobainika kushiriki vitendo vinavyozalisha migogoro hiyo.

Aidha, ameeleza kuwa ardhi ni rasilimali muhimu kwa maendeleo ya wananchi na taifa kwa ujumla, hivyo ni lazima isimamiwe kwa uadilifu, uwazi na weledi ili kuondoa malalamiko yanayoendelea kujitokeza katika maeneo mbalimbali nchini.

Dkt. Mwigulu ameonya kuwa migogoro ya ardhi ikiendelea kuachwa bila kutatuliwa inaweza kuathiri umoja wa wananchi na kuleta uhasama usio wa lazima, akisisitiza kuwa kila taasisi inayohusika na usimamizi wa ardhi inapaswa kutekeleza wajibu wake kwa kuzingatia sheria, kanuni na maslahi ya wananchi.

Aidha  amewataka viongozi na watendaji wa sekta hiyo kuhakikisha wanashughulikia kwa haraka kero za ardhi zinazowakabili wananchi ili kuimarisha amani, mshikamano na maendeleo ya taifa.



 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Dkt. Mahmoud Thabit Kombo amekutana na  Jumuiya ya Diaspora ya Tanzania wanaoishi katika Jamhuri ya Korea na kuwahimiza kuendelea kuwa mabalozi wazuri wa Tanzania kwa kuitangaza nchi na fursa mbalimbali zilizopo katika sekta za uwekezaji, biashara na utalii. 

Akizungumza katika mkutano uliofanyika  jijini Seoul, Mei 31, 2026,  Balozi Dkt. Kombo alisisitiza umuhimu wa Watanzania wanaoishi nje kuifahamu vizuri nchi wanayoishi, ikiwemo tamaduni zake, lugha, sheria na mifumo ya kijamii ili waweze kujumuika kwa urahisi na kujenga uhusiano chanya unaoweza kuleta manufaa kwa Taifa. 

Alifafanua kuwa uelewa wa mazingira ya nchi mwenyeji huwasaidia diaspora kutambua fursa za kiuchumi na kijamii ambazo zinaweza kuwanufaisha wao pamoja na kuimarisha ushirikiano kati ya Tanzania na nchi husika. 

Pia aliwahimiza kutumia majukwaa yao mbalimbali ya kitaaluma, kijamii na kibiashara kuitangaza Tanzania pamoja na fursa zinazopatikana katika nchi wanazoishi. Alibainisha kuwa kupitia mitandao na ushirikiano wao, diaspora wanayo nafasi kubwa ya kuvutia wawekezaji, watalii na washirika wa maendeleo kuwekeza na kushirikiana na Tanzania. 

Pia alitoa wito kwa Diaspora ambao ni wanafunzi wa elimu ya juu kujikita katika kufanya tafiti zinazolenga kutatua changamoto mbalimbali zilizopo nchini hususan katika sekta za afya, maji, elimu na mazingira. 

Kadhalika alitoa rai kwa Diaspora hao kuendelea kudumisha umoja, uzalendo na maadili mema ili kuendeleza taswira chanya ya Tanzania nchini Korea na kimataifa kwa ujumla. 

Kwa upande wake, Rais wa Jumuiya hiyo Bi. Eliusta Filikunjombe alieleza utayari wao wa kuendelea kushirikiana na Serikali katika kutangaza fursa na kuimarisha mahusiano ya watu kwa watu kati ya Tanzania na Jamhuri ya Korea. 

Awali akizungumza, Balozi wa Tanzania nchini Korea, Mhe. Noel Kaganda alisema idadi ya Diaspora wa Tanzania nchini humo inafikia 300 ambayo inajumuisha wafanyakazi, wafanyabiashara na wanafunzi. 

Mhe. Balozi Dkt Kombo yupo nchini Korea kwa ajili ya kushiriki Mkutano wa Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Korea na Afrika.














 

*Kinara wa Mageuzi Sekta ya Mafuta
*Ampongeza Rais Samia kwa Uchapakazi, Asema Tanzania Itashinda Changamoto ya Mafuta

Na Mwandishi Wetu
KATIKA ulimwengu wa biashara na uchumi wa kisasa, viongozi wachache huweza kuunganisha utaalamu, ubunifu, uzalendo na uwezo wa kuleta matokeo yanayoonekana ndani ya muda mfupi. Tanzania imebahatika kuwa na baadhi ya viongozi wa aina hiyo ambao kupitia maarifa yao wameendelea kutoa mchango mkubwa katika maendeleo ya taifa.

Miongoni mwao ni Dk. Sajad Habib Rai, mtaalamu mwenye uzoefu wa zaidi ya miaka 20 katika sekta ya mafuta, usafirishaji, manunuzi, teknolojia ya habari na usimamizi wa biashara.

Kupitia nafasi yake kama Meneja Mkazi wa Mansoor Industries Limited, Dk. Sajad ameonyesha uwezo mkubwa wa kusimamia operesheni za biashara huku akihakikisha kampuni inaendelea kukua na wakati huo huo kuunga mkono jitihada za Serikali za kuongeza mapato ya taifa.

Safari ya Mafanikio
Dk. Sajad, mwenye umri wa miaka 47, alianza safari yake ya kitaaluma kwa misingi ya nidhamu, kujifunza kwa bidii na kujituma kazini. Tangu akiwa kijana alionyesha uwezo mkubwa wa uongozi na hamu ya kutafuta suluhisho kwa changamoto mbalimbali zinazokabili taasisi na jamii.

Anasema Tanzania imebahatika kuwa na viongozi wenye maono tangu ilipopata uhuru mwaka 1961, na anaamini maendeleo ya taifa yanahitaji viongozi wanaoweka mbele maslahi ya wananchi na kufanya maamuzi yenye manufaa ya muda mrefu.

Rais Samia na Maendeleo ya Uchumi
Dk. Sajad anamtaja Rais Samia Suluhu Hassan kama mmoja wa viongozi waliobeba matumaini makubwa ya Watanzania katika kipindi hiki.

Kwa mujibu wake, uongozi wa Rais Samia umeleta ari mpya katika uwekezaji, utendaji wa serikali na usimamizi wa sekta mbalimbali za uchumi.

"Tunajivunia kuwa na kiongozi mwenye maono na anayefanya kazi kwa karibu na wananchi. Rais Samia ameonyesha uwezo mkubwa wa kuisimamia Tanzania katika kipindi kigumu cha changamoto za kiuchumi duniani," anasema.

Kauli hiyo inaakisi namna anavyounga mkono juhudi za serikali katika kuhakikisha uchumi wa taifa unaendelea kuwa imara licha ya changamoto zinazotokana na mabadiliko ya bei za mafuta na migogoro ya kimataifa.

Mbunifu wa Mfumo wa Kudhibiti Ukwepaji Kodi
Katika sekta ya mafuta, Dk. Sajad amejizolea sifa kama mmoja wa wataalamu wenye mawazo ya kimkakati yanayolenga kuleta uwazi na ufanisi katika biashara hiyo.

Kupitia uzoefu wake katika usafirishaji wa mafuta, usimamizi wa bohari na operesheni za biashara, aliweza kubaini mianya iliyokuwa ikisababisha Serikali kupoteza mapato kupitia ukwepaji wa kodi.

Moja ya michango yake mikubwa ni kupendekeza mfumo wa ulipaji kodi kwa waingizaji wa mafuta kabla bidhaa hizo hazijaingia sokoni. Mfumo huo ulisaidia kwa kiasi kikubwa kudhibiti mianya ya ukwepaji kodi na kuongeza uwezo wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kukusanya mapato kwa ufanisi zaidi.

Kwa mujibu wake, kabla ya kuanzishwa kwa mfumo huo kulikuwa na changamoto ya baadhi ya wafanyabiashara kutumia mianya ya kisheria kukwepa kodi. Hata hivyo, baada ya kuanzishwa kwa mfumo wa kukadiria kodi mapema kabla ya mafuta kuingia sokoni, hali ilibadilika kwa kiasi kikubwa.

"Mfumo huu umeongeza uwajibikaji na kusaidia kuondoa mazingira ya ujanja ujanja yaliyokuwa yanapelekea upotevu wa mapato ya taifa," anasema.

Anasisitiza kuwa mafanikio hayo yanaonyesha namna sekta binafsi inaweza kuwa mshirika muhimu wa serikali katika kuleta maendeleo ya taifa.

Kiongozi wa Biashara ya Mafuta
Katika Mansoor Industries Limited, Dk. Sajad anasimamia shughuli mbalimbali ikiwemo manunuzi, operesheni, usimamizi wa miradi na mipango ya biashara.

Kampuni hiyo inajishughulisha na biashara ya mafuta ya petroli na dizeli, huku pia ikimiliki Bohari ya Mafuta ya MOIL iliyopo Kigamboni, Dar es Salaam.

Uzoefu Mkubwa Katika TEHAMA
Mbali na sekta ya mafuta, Dk. Sajad ana uzoefu mkubwa katika teknolojia ya habari na mawasiliano.

Mwaka 2003 hadi 2004 alihudumu kama Meneja wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika Nyanza Bottling Company Ltd, ambapo alisimamia mifumo yote ya TEHAMA ya kampuni.

Katika kipindi hicho alifanikiwa kuboresha seva, mifumo ya barua pepe na miundombinu ya mtandao. Kupitia ubunifu wake, matatizo ya kiufundi yalipungua kwa asilimia 95 kutokana na matengenezo ya mara kwa mara na usimamizi bora wa mifumo ya taarifa.

Aidha, alitoa mafunzo kwa wafanyakazi kuhusu matumizi sahihi ya mifumo ya kompyuta na usalama wa taarifa, hatua iliyoongeza ufanisi wa kazi ndani ya kampuni.

Mafanikio Katika Manunuzi na Ugavi
Katika taaluma ya manunuzi na ugavi, Dk. Sajad aliwahi kuhudumu kama Meneja wa Manunuzi ambapo alisimamia mzunguko mzima wa manunuzi ya ndani na nje ya nchi.

Kupitia mikakati yake ya manunuzi na majadiliano na wasambazaji, alipunguza gharama za kampuni kwa asilimia 25.

Pia aliweka mifumo madhubuti ya ufuatiliaji wa bidhaa, kupanga viwango vya chini vya bidhaa ghala na kuboresha makadirio ya mahitaji ya malighafi. Uwezo wake huo ulimwezesha kutunukiwa Tuzo ya Forecast kutoka Coca-Cola Swaziland.

Mafanikio Katika Masoko na Mauzo
Dk. Sajad pia ametoa mchango mkubwa katika sekta ya masoko na mauzo. Akiwa Msimamizi wa Masoko wa Nyanza Bottling Company Ltd, aliongoza kampeni mbalimbali zilizosaidia kuongeza mauzo na kuimarisha ushindani wa kampuni sokoni.

Moja ya mafanikio yake makubwa ni kuanzisha programu ya VIP Club iliyoongeza mauzo kwa zaidi ya asilimia 216. Aidha, alisimamia utekelezaji wa programu za EDS na ITMO zilizofanikisha ufanisi wa asilimia 99.36.

Kupitia uwezo wake wa kujenga mahusiano bora ya biashara, alifanikiwa kuwabadilisha mawakala 75 kutoka kuwa wauzaji wa bidhaa mchanganyiko hadi washirika rasmi wa kampuni.

Tanzania na Changamoto ya Mafuta Duniani
Katika kipindi hiki ambacho dunia inakabiliwa na changamoto za upatikanaji wa mafuta kutokana na migogoro ya Mashariki ya Kati, Dk. Sajad anaamini Tanzania ipo katika nafasi nzuri zaidi kuliko mataifa mengi.

Anasema changamoto ya mafuta ni suala la kimataifa, lakini Tanzania imeweza kuvuka kipindi hicho kwa utulivu kutokana na usimamizi mzuri wa serikali na ushirikiano wa karibu kati ya sekta binafsi na taasisi za umma.

Kwa mujibu wake, baadhi ya nchi alizotembelea hivi karibuni zimekumbwa na uhaba wa mafuta uliosababisha kupanda kwa bei za tiketi za ndege, kupunguzwa kwa safari za ndege na mgao wa nishati. Hata hivyo, Tanzania imeendelea kuwa na akiba ya kutosha ya mafuta huku bei zikiwa nafuu ukilinganisha na baadhi ya mataifa jirani.

Kiongozi Anayejali Watu
Mbali na mafanikio yake ya kitaaluma, Dk. Sajad anatambulika kama kiongozi anayejali maendeleo ya wafanyakazi wake.

Anaamini mafanikio ya taasisi yoyote yanategemea uwepo wa timu yenye mshikamano, nidhamu na uwajibikaji. Kwa miaka yote aliyohudumu katika nafasi mbalimbali za uongozi, amekuwa mstari wa mbele kujenga mazingira bora ya kazi, kutoa mafunzo na kuwapa wafanyakazi nafasi ya kukuza vipaji vyao.

Historia ya Elimu na Uongozi
Safari yake ya uongozi ilianza mapema alipokuwa Meneja wa Tawi la Aptech Learning kuanzia mwaka 2000 hadi 2002. Katika nafasi hiyo alisimamia shughuli zote za tawi ikiwemo mauzo, huduma kwa wateja na usajili wa wanafunzi.

Kitaaluma, Dk. Sajad alipata elimu yake ya sekondari katika Shule ya Sekondari Mwanza alikosoma masomo ya uchumi kati ya mwaka 1993 na 1995. Elimu yake ya msingi aliipata katika Shule ya Msingi Nyakahoja, huku pia akisoma katika Shule ya Limitless Learning.

Hitimisho
Kwa kuangalia mchango wake katika sekta ya mafuta, TEHAMA, manunuzi, masoko na usimamizi wa biashara, Dk. Sajad Habib Rai ni miongoni mwa wataalamu wa Kitanzania waliochangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya sekta binafsi na uchumi wa taifa.

Kupitia ubunifu wake katika kuboresha mifumo ya ukusanyaji kodi, kuimarisha ufanisi wa biashara na kuunga mkono juhudi za serikali, ameendelea kuwa mfano wa viongozi wanaotumia taaluma zao kuleta mabadiliko chanya kwa jamii na taifa kwa ujumla.

Zaidi ya wafugaji 200 wa Kanda ya Ziwa wamepata elimu kuhusu matumizi ya mifumo ya kidigitali katika sekta ya mifugo, iliyotolewa na kampuni ya climb Up Limited, ili kuwawezesha wafugaji kuongeza tija katika uzalishaji wa mifugo bora na kuachana na mbinu za ufugaji  ambazo zimepitwa na wakati.

Hayo yameelezwa na Afisa Masoko wa kampuni hiyo, Jackline Cosmas, Mei 31 mkoani Shinyanga wakati wa kuhitimisha Maonyesho ya Mifugo ya Kanda ya Ziwa yaliyofanyika kwa muda wa siku mbili.

Baadhi ya wafugaji waliotembelea banda la Climb Up Limited na kupata mafunzo hayo wamesema elimu waliyoipata itawasaidia kubadilisha mtazamo wao kuhusu ufugaji, kutoka katika mbinu za jadi na kuelekea ufugaji wa kisasa unaotumia teknolojia kwa ajili ya kuongeza uzalishaji na ufanisi.





 

Na Said Mwishehe,Michuzi TV

HATIMAYE Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi mahiri wa Rais Dk.Samia Suluhu Hassan imetangaza rasmi kwamba kuanzia Julai 1 mwaka huu wa 2025 nchi yetu ya Tanzania itaanza utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Wakati utekelezaji huo ukitarajiwa kuanza tarehe hiyo ya Julai 1, tayari upo msingi imara wa kisera, kitaasisi na kiutekelezaji unaolenga kuharakisha mageuzi ya kiuchumi, kijamii na kiutawala kwa miongo ijayo. 

Katika kikao chake kilichofanyika Dar es Salaam hivi karibuni chini ya Mwenyekiti wake, Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, Tume ya Taifa ya Mipango iliidhinisha miongozo na mifumo muhimu ya kusimamia utekelezaji wa Dira 2050 pamoja na kuelekeza kuharakishwa kwa miradi mikubwa ya kimkakati itakayokuwa nguzo kuu ya ukuaji wa uchumi wa Taifa.

Pamoja na kuidhinisha Mwongozo wa Kitaifa wa Mipango, Mwongozo wa Kitaifa wa Uidhinishaji wa Miradi ya Maendeleo, Mwongozo wa Kitaifa wa Ufuatiliaji na Tathmini ya Miradi ya Maendeleo na Mkakati wa Mawasiliano wa Dira 2050, Tume imeweka msisitizo maalum katika utekelezaji wa miradi mikubwa ya uwekezaji inayotarajiwa kuchochea mabadiliko ya kimuundo katika uchumi wa Tanzania.


Miradi hiyo ni pamoja na Mradi wa Kuchakata Gesi Asilia kuwa Kimiminika (LNG), Mradi Unganishi wa Chuma cha Liganga na Makaa ya Mawe ya Mchuchuma, Mradi wa Kabanga Nickel pamoja na Kiwanda cha Usafishaji Kahama, na Mradi wa Magadi Soda wa Engaruka. 

Kwa pamoja, miradi hiyo inawakilisha uwekezaji wenye thamani ya zaidi ya shilingi trilioni 120, sawa na takribani dola za Marekani bilioni 47.

Miradi hiyo imeainishwa kama sehemu muhimu ya utekelezaji wa Dira 2050 kwa sababu ina uwezo wa kuvutia uwekezaji mkubwa wa ndani na nje, kuongeza ajira, kuimarisha mapato ya Serikali, kukuza mauzo ya nje, kuongeza matumizi ya teknolojia za kisasa na kuimarisha ushindani wa Tanzania katika uchumi wa kikanda na kimataifa.

Mradi wa LNG unatarajiwa kuwa kichocheo kikubwa cha ukuaji wa sekta ya nishati na mapato ya fedha za kigeni. 

Liganga na Mchuchuma vinatarajiwa kuweka msingi wa maendeleo ya viwanda kwa kuongeza uzalishaji wa chuma na nishati nchini. Kabanga Nickel inaipa Tanzania nafasi ya kushiriki kikamilifu katika uchumi wa kijani unaochochewa na ongezeko la mahitaji ya madini muhimu kwa utengenezaji wa betri na teknolojia za nishati safi duniani. 


Nayo Engaruka inafungua fursa mpya katika sekta ya kemikali na viwanda vinavyotegemea malighafi za ndani.

Kwa kuzingatia malengo ya Dira 2050 ya kufikia uchumi wa takribani dola trilioni moja, miradi hiyo siyo uwekezaji wa kawaida bali ni injini za mageuzi ya kiuchumi. 

Hivyo uamuzi wa Tume ya Taifa ya Mipango wa kuipa kipaumbele utekelezaji wake unaashiria dhamira ya Serikali ya kuhakikisha Dira 2050 inatafsiriwa katika matokeo halisi yatakayoongeza tija, ajira, ustawi wa wananchi na ushindani wa Taifa katika miaka ijayo.

Pamoja na hayo ukweli ni kwamba kuanza kwa utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inaonesha dhamira,kiu na shauku ya Rais Dk.Samia Suluhu Hassan kuona nchi yetu inapiga hatua zaidi katika kuleta maendeleo, kuboresha hali za maisha ya wananchi na kubwa zaidi kuifanya Tanzania kuwa injini ya kukuza uchumi wake kupitia rasilimali zake .

Unapoiangalia Dira ya Taifa ya Maendeleo unaiona Tanzania tuitakayo na safari ya kuelekea huko inaanza sasa. Hongera Serikali ya Awamu ya Sita kwa hatua hii inayowasha taa ya kijani yenye matumaini makubwa kwa Watanzania.

Lakini kwa muda mrefu Watanzania tumekuwa tukiitamani Tanzania itakayokuwa na uwezo mkubwa wa kuajiri watu wake kupitia sekta mbalimbali na katika Dira hiyo imeeleza kwa kina namna ambavyo nchi inavyokwenda kuimarisha sekta hizo kama mkakati wa kutengeneza fursa za ajira kwa Watanzania.

Kwa mfano Tume ya Taifa ya Mipango chini ya Rais Dk.Samia Suluhu Hassan katika kikao chake cha Mei 26 pamoja na mambo mengine pia imeidhinisha sekta za kipaumbele 12 wakati wa utekelezaji wa dira hiyo.

Sekta hizo ni ya kilimo idadi ya viashiria vya upimaji katika mabano ni (15), viwanda na ujenzi (10), Madini na Nishati(10), Utalii(5), michezo na Sanaa(9), sekta ya ubunifu na maudhui ya kidigitali(2) wakati sekta ya miliki ,aridhi na maendeleo ya miji(13)

Pia sekta nyingine ni biashara na uwekezaji(12), Elimu(54), hifadhi za jamii,kazi na ustawi wa jamii(34), uchumi wa bluu(18) pamoja na sekta ya Sayansi,teknolojia,ubunifu na uchumi wa digitali(24).

Unapoangalia sekta hizo ambazo zimepewa kipaumbele katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 utabaini mkakati uliopo kama nchi ni kuhakikisha Tanzania inaendelea kufungua fursa zaidi ambazo kila mmoja atashiriki katika shughuli za kiuchumi na hatimaye kwa pamoja kubadilisha maisha yetu kutoka tuliyonayo sasa na kuwa na maisha bora zaidi.

Na kwa kuwa dira hiyo imelenga kubadilisha maisha yetu ni matumaini yangu wananchi wote na wa rika na kada zote tunaowajibu wa kuungana na Rais Dk.Samia na Serikali anayoiongoza katika kuwa sehemu ya safari ya kutekeleza dira hiyo ambayo ikifanikiwa kizazi kilichopo sasa na kijacho kitakuwa kwenye ile nchi ya ahadi ya asali na maziwa.

Kupitia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inaonesha jinsi ambavyo inakwenda kuinua uchumi wa mtu mmoja mmoja na lengo ni kuwezesha pamoja na kuwa na ukuaji wa uchumi kwa ujumla kama Taifa lakini pia uchumi wa kila mmoja wetu nao ukue.Ndio mpango uliopo.

Binafsi sina shaka na Rais Dk.Samia katika kusimamia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kwani kwa dhamira yake na utashi wake ndio aliyetoa maelekezo ya kuandikwa kwa Dira hiyo kazi ambayo ilifanyika kwa weledi mkubwa na kupita katika hatua mbalimbali na hatimaye sasa utekelezaji wake unakwenda kuanza rasmi.

Hata hivyo nitoe rai kwa Vyama vya siasa nao wanapaswa kuwa sehemu ya kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wa dira hiyo.Ni matumaini yangu kama ilivyo kwa CCM Ilani yake imeakisi kwa kiasi kikubwa yaliyomo katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Hivyo kwa vyama vya siasa vya upinzani kuakisi yaliyomo katika Dira hiyo kupitia Ilani zao.Lakini kwa kuwa utekelezaji wa dira unaanza Julai 1,2026 ni vema wanasiasa wetu bila kujali itikadi ya vyama wakaungana na Watanzania wote kuitekeleza dira hiyo.


Simu 0713833822


Mwisho



 

Kamati ya Kudumu ya Bunge inayosimamia masuala ya Utawala, Katiba na Sheria imeeleza kuridhishwa na hatua zilizofikiwa katika utekelezaji wa miradi ya uwekezaji ndani ya Eneo Maalum la Kiuchumi la Bagamoyo – BEMC. Kauli hiyo imetolewa baada ya kamati kufanya ziara ya ukaguzi ili kujionea maendeleo ya shughuli mbalimbali zinazosimamiwa na Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalum ya Kiuchumi Tanzania, TISEZA.

Eneo la BEMC lilianzishwa kisheria kupitia Tangazo la Serikali Na. 123 la tarehe 24 Mei 2013. Lina jumla ya hekta 9,800, ambapo hekta 887 zimetengwa mahsusi kwa ajili ya Bandari ya kisasa ya Mbegani. Sehemu iliyobaki, yenye hekta 8,903, inatumiwa kwa shughuli za uwekezaji. Mradi huu unatajwa kuwa wa kimkakati kitaifa na unalenga kukuza sekta ya viwanda, biashara na uchumi kwa ujumla.

Katika Mpango wa Maendeleo wa Taifa, BEMC umetambuliwa kama moja ya nguzo zitakazosaidia Tanzania kufikia lengo la kuwa na uchumi wenye thamani ya dola trilioni moja ifikapo 2050. Kufikia Mei 2026, wawekezaji 24 tayari walikuwa wameshapatiwa maeneo na kuanza utekelezaji wa miradi yao. Miradi hiyo ipo katika hatua tofauti kama ujenzi wa viwanda, mabanda ya uzalishaji, uzio pamoja na miundombinu wezeshi.

Wakati wa ziara hiyo, Kamati ilisema imefurahishwa na kasi ya ujenzi na uwekezaji unaoendelea. Miongoni mwa miradi iliyotajwa kuvutia ni kiwanda cha Sinovest Industry Investment Limited kitakachozalisha nguo na bidhaa za nguo. Kiwanda hicho kimejengwa kwenye eneo la mita za mraba 210,080, sawa na hekta 21. Mpaka Mei 2026, uwekezaji uliofanyika ulifikia dola milioni 7 za Marekani, sawa na zaidi ya shilingi bilioni 21. Kinatarajiwa kuanza uzalishaji rasmi mwishoni mwa Juni 2026.

Kukamilika kwa kiwanda hicho kutaleta ajira nyingi. Awamu ya kwanza itazalisha ajira 1,000 za moja kwa moja, na awamu ya pili itaongeza ajira 500. Kiwanda kitatumia mashine za kisasa kuzalisha nguo zenye ubora wa kimataifa kwa ajili ya masoko ya Marekani na Ulaya.

Uwekezaji wa aina hiyo unachangia kwa kiasi kikubwa pato la Taifa, unaongeza thamani ya bidhaa za viwandani, pamoja na kuboresha kipato cha wananchi wa Bagamoyo, Mkoa wa Pwani na Tanzania nzima.

TISEZA inalenga kuhakikisha maeneo yote maalum ya uwekezaji yanatumika kikamilifu ili kuvutia mitaji na kuleta tija kwa wananchi. Lengo ni kuwafanya Watanzania wanufaike na fursa za uwekezaji katika sekta mbalimbali. Uwekezaji unabaki kuwa chombo muhimu cha kutoa ajira, kuvutia mitaji kutoka nje, kuhamisha teknolojia na kuimarisha msingi wa viwanda nchini.

Maendeleo yanayoonekana BEMC yanaonyesha nia ya dhati ya Serikali katika kuboresha mazingira ya uwekezaji na kusukuma utekelezaji wa miradi mikubwa yenye maslahi mapana kwa wananchi na Taifa.







-Pia yabainisha mkakati wa mageuzi katika mifumo ya utawala na utumishi wa umma

-Utekelezaji Dira 2050 kuanza kutekelezwa rasmi kuanzia Julai 1, 2026


Na Said Mwishehe,Michuzi TV


TUME ya Mipango ya Taifa imeidhinisha miongozo minne itakayotumika katika kusimamia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 utakaoanza Julai 1 mwaka 2026.

Akizungumza leo Mei 31 katika mkutano wa waandishi wa habari uliofanyika Ikulu jijini Dar es Salaam,Waziri wa Mipango na Uewekezaji Profesa Kitila Mkumbo amesema miongozo hiyo imetolewa baada ya Tume ya Taifa ya Mipango chini ya Mwenyekiti wake Rais Dk.Samia Suluhu Hassan kufanya kikao Mei 26 mwaka huu.

“Katika kikao hicho, pamoja na mambo mengine, Tume ya Taifa ya Mipango ilijadili na kuidhinisha miongozo/mikakati minne itakayotumika katika kusimamia tekelezaji wa Dira 2050 utakaonza Julai 1, 2026.”

Profesa Mkumbo ameitaja miongozo hiyo ni Mwongozo wa Kitaifa wa Mipango,Mwongozo wa Kitaifa wa Uidhinishaji wa Miradi ya Maendeleo, Mwongozo wa Kitaifa wa Ufuatiliaji na Tathmini ya Miradi ya Maendeleo,Mkakati wa Mawasiliano wa Dira 2050 wa Miaka Mitano 2026/27 - 2030/31.

“Ilipojadili Muongozo wa Kitaifa wa Ufuatiliaji na Tathmini ya Miradi ya Maendeleo, Tume ya Taifa ya Mipango iliidhinisha maeneo makubwa matatu ya kimkakati yanayohitaji mageuzi yenye viashiria vya upimaji 142.

“Maeneo haya na idadi ya viashiria vyake ya upimaji ni Mageuzi katika mifumo ya utawala na utumishi wa umma (Governance and civil service reforms, viashiria 13), Mageuzi katika uwekezaji na uzalishaji (structural transformation for investment, infusion and productivity, viashiria 53) pamoja na Mageuzi katika maendeleo ya kijamii, kiuchumi na mazingira (socio economic outcomes, viashiria 76)

Ameongeza pia Tume ya Taífa ya Mipango ilidhinisha sekta za kipaumbele 12 kama zilivyainishiwa katika Mpango wa Nne wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka
Mitano yenye viashiria vya upimaji 206

Amefafanua katika sekta ya kilimo idadi ya viashiria vya upimaji katika mabano ni 15, viwanda na ujenzi (10), Madini na Nishati(10), Utalii(5), michezo na Sanaa(9), sekta ya ubunifu na maudhui ya kidigitali(2) wakati sekta ya miliki ,aridhi na maendeleo ya miji(13)

Pia katika sekta ya biashara na uwekezaji(12), Elimu(54), hifadhi za jamii,kazi na ustawi wa jamii(34), uchumi wa bluu(18) pamoja na sekta ya Sayansi,teknolojia,ubunifu na uchumi wa digitali(24).

Akieleza zaidi Profesa Mkumbo ameeleza pia Tume ya Taifa ya Mipango ilielekeza kuwa Sekretariati ya Tume ijielekeze na kujikita katika kusimamia utekelezaji wa mipango ya maendeleo.

Aidha, katika kumarisha simamizi wa utekelezaji wa mipango ya maendeleo, Mwenyekiti
wa Tume alielekeza kuwa, wakati ambapo Tume haikutani katika vikao vya kawaida chini yake, wajumbe wa Tume watajigeuza kuwa Ofisi ya Usimamizi wa Utekelezaji wa Mipango (Delivery Bureau) na vikao vyake vitasimamiwa na
Makamu Mwenyekiti wa Tume.

Ameongeza Tume ya Taifa ya Mipango ilielekeza kukamilishwa kwa haraka kwa majadiliano kati ya Serikali na wawekezaji kuhusu miradi ya kimkakati ya uwekezaji inayotarajiwa kujenga msingi ya kukuza uchumi na kuchochea ajira kama sehemu muhimu ya utekelezaji wa Dira 2050 na Mpango wa Nne wa Taifa wa Maendeleo ya Miaka Mitano (2026/27 - 2030/31).

Amitaja miradi hiyo ni Mradi unganishi wa chuma cha Liganga na makaa ya mawe ya Mchuchuma, Mradi wa magadi soda wa Engaruka, Mradi wa kuchakata gesi asilia kuwa kimiminika (LNG), Mradi wa nikeli wa Kabanga (Kabanga Nickel Project) na kiwanda cha usafishaji cha Kahama.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji Mhe. Profesa Kitila Alexander Mkumbo akizungumza na Waandishi wa Habari kuhusu kuanza Utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 (DIRA2050), tarehe 31 Mei, 2026 Ikulu, Dar es Salaam.



Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani Mkoa wa Arusha, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Zauda Mohamed, ameongoza mafunzo maalum kwa walimu wa vyuo vya udereva jijini Arusha, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuimarisha ubora wa mafunzo ya udereva na kuongeza usalama barabarani Pamoja na Kuimarisha matumizi ya Tehama katika Usimamizi wa vyuo hivyo.

Mafunzo hayo yanaendelea kutolewa katika Chuo cha Ufundi Arusha (Arusha Technical College - Arusha Tech), ambapo walimu hao wanapatiwa ujuzi na mbinu za kisasa zitakazowawezesha kuandaa madereva wenye sifa, weledi na uelewa unaokidhi mahitaji ya sheria, kanuni na taratibu za usalama barabarani za sasa.

Akizungumza baada ya mafunzo hayo, ACP Zauda Mohamed amesema lengo la Kikosi cha Usalama Barabarani ni kuhakikisha walimu wa vyuo vya udereva wanakuwa na uwezo wa kuzalisha madereva wenye viwango vinavyokubalika kitaifa na kimataifa.

“Tunataka kuona madereva wanaopata mafunzo kutoka kwa walimu hawa wanakuwa na sifa stahiki na kuzingatia sheria za usalama barabarani. Hii itasaidia kupunguza ajali za barabarani na hatimaye kuokoa maisha ya wananchi,” amesema ACP Zauda.

Ameongeza kuwa kikosi hicho kinaendelea kuweka mkazo katika utoaji wa elimu na mafunzo kwa wadau mbalimbali wa sekta ya usafirishaji ili kuhakikisha ajali za barabarani zinapungua kwa kiwango kikubwa, na ikiwezekana kutokomezwa kabisa.

Pia amewataka walimu hao kuendelea kuboresha mbinu za ufundishaji na kuzingatia mabadiliko ya teknolojia pamoja na mahitaji ya soko la ajira, akibainisha kuwa kwa sasa mahitaji ya madereva wenye taaluma na ujuzi wa kutosha yanaongezeka ndani na nje ya nchi.

Kwa upande wao, baadhi ya walimu wa vyuo vya udereva waliohudhuria mafunzo hayo wamelishukuru Jeshi la Polisi kupitia Kikosi cha Usalama Barabarani Mkoa wa Arusha kwa kuendelea kuwawezesha kitaaluma mara kwa mara.

Wamesema mafunzo hayo yanawajengea uwezo wa kufundisha kwa viwango vya juu zaidi na kuwasaidia kuzalisha madereva wenye umahiri unaokidhi vigezo vya kitaifa na kimataifa.






WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba leo Jumapili Mei 31, 2026 amekagua ujenzi wa Barabara ya Noranga (Doroto)–Itigi (Mlongojii) yenye urefu wa kilomita 25 inayojengwa katika Halmashauri ya Itigi, Wilaya ya Manyoni mkoani Singida kwa gharama ya shilingi bilioni 29.6.

Akipokea taarifa ya utekelezaji wa mradi huo kutoka kwa Mkurugenzi wa Miradi wa Wakala ya Barabara Tanzania (TANROADS), Mhandisi Japherson Nnko, Dkt. Mwigulu alielezwa kuwa hadi Mei 30, 2026 mradi huo umefikia asilimia 83.25 ya utekelezaji ambapo kilomita 20.2 zimekamilika kwa kiwango cha lami huku kilomita 4.8 zilizobaki zikiwa zimejengwa hadi tabaka la juu la msingi na zinatarajiwa kukamilika Juni 30, 2026.

Mhandisi Nnko alisema kipande hicho ni sehemu ya Barabara ya Mbeya–Chunya–Makongolosi–Rungwa–Itigi–Mkiwa yenye urefu wa kilomita 524 inayounganisha mikoa ya Mbeya, Singida na Tabora na ambayo inatarajiwa kuimarisha usafirishaji wa watu, bidhaa na mazao katika ukanda huo.

Alisema mradi huo unagharamiwa kwa asilimia 100 na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na unatekelezwa na Kampuni ya China Henan International Cooperation Group Co. Ltd (CHICO) kutoka China kwa gharama ya shilingi 29.6 bila VAT.

Aidha, alisema kazi za ujenzi zilianza Septemba 16, 2022 na zinatarajiwa kukamilika Agosti 7, 2026 baada ya mkandarasi kuongezewa muda wa utekelezaji kwa mujibu wa mkataba.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, hadi Mei 30, 2026 mkandarasi alikuwa amelipwa shilingi bilioni 12.9 na alikuwa anadai shilingi bilioni 3.84. Aidha, Mhandisi Mshauri alikuwa amelipwa shilingi bilioni 1.49 na anadai shilingi milioni 586.6.

Pia, wananchi 578 ambao mali zao ziliathiriwa na mradi huo wamelipwa fidia ya jumla ya shilingi milioni 721.4 kwa mujibu wa sheria.

Katika utekelezaji wake, mradi huo umezalisha ajira 305 ambapo ajira 278 sawa na asilimia 91 zimetolewa kwa wazawa na ajira 27 sawa na asilimia 9 zimetolewa kwa wageni.













Serikali ya Tanzania imesaini mkataba na Kampuni ya Lindi Jumbo Limited kwa ajili ya kuwezesha ushiriki rasmi wa Serikali katika Mradi wa uchimbaji wa madini ya kinywe wa Lindi Jumbo kupitia kampuni ya ubia ya Ndovu Graphite Limited, hatua inayotajwa kuwa mafanikio makubwa kwa sekta ya madini na mkakati wake kupitia ajenda ya madini nchini.

Hafla ya utiaji saini iliyofanyika jana katika Kijiji cha Matambarale, Wilaya ya Ruangwa mkoani Lindi, imeiwezesha Serikali kupata asilimia 16 ya hisa huru zisizohafifishwa thamani katika mradi huo, huku Lindi Jumbo Limited ikibaki na umiliki wa asilimia 84.

Akizungumza katika hafla hiyo, Waziri wa Madini, Mheshimiwa Anthony Mavunde, alisema makubaliano hayo ni hatua ya kihistoria katika kuhakikisha Watanzania wananufaika moja kwa moja na rasilimali za taifa kupitia ushiriki wa Serikali katika uwekezaji wa madini.

Kwa mujibu wa makubaliano hayo, Serikali itashiriki katika mradi bila kubeba gharama za awali za uwekezaji, huku ikipata gawio, kushiriki katika maamuzi ya kimkakati pamoja na kuongeza usimamizi wa mapato yatokanayo na madini.

Mheshimiwa Mavunde alisema makubaliano hayo yanaonesha mabadiliko ya namna Tanzania inavyosimamia rasilimali zake za madini, akisisitiza kuwa nchi inapaswa kuondokana na utegemezi wa kuuza malighafi pekee.

“Serikali chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan imeendelea kuimarisha taswira ya Tanzania kama eneo tulivu na rafiki kwa wawekezaji,” alisema. “Kupitia sheria zilizo wazi, taasisi zinazoendelea kuimarika na dira ya muda mrefu ya uchumi, wawekezaji sasa wanaiona Tanzania siyo tu kama chanzo cha madini, bali mshirika wa kuaminika katika uwekezaji wenye usawa na endelevu.”

Waziri huyo alieleza kuwa Kinywe imeendelea kuwa madini muhimu duniani kutokana na matumizi yake katika utengenezaji wa betri za magari ya umeme, teknolojia za nishati safi na mabadiliko ya mfumo wa matumizi ya nishati duniani.

Aliitaja Kinywe kama “dhahabu nyeusi” ya uchumi wa kisasa, akisema uchumi wa dunia utaendelea kutegemea madini mkakati yanayochochea maendeleo ya teknolojia na mifumo ya nishati ya kijani.

Kwa mujibu wa Mheshimiwa Mavunde, Mradi wa Lindi Jumbo ni miongoni mwa miradi yenye kiwango cha juu zaidi cha ubora wa kinywe duniani, ukiwa na wastani wa asilimia 17.9 ya Total Graphitic Carbon (TGC), hali inayoufanya kuwa moja ya migodi bora zaidi ya kinywe barani Afrika. Mradi huo unatarajiwa kuzalisha takribani tani 40,000 za kinywe kwa mwaka katika kipindi cha miaka 24 ya uhai wa mgodi.

Waziri huyo pia alisisitiza dhamira ya Serikali katika kuendeleza uchumi wa viwanda na kuongeza thamani ya madini, akisema Tanzania inalenga kuhamasisha uwekezaji katika uchakataji wa madini, utengenezaji wa betri na viwanda vinavyotegemea kinywe pamoja na madini mengine ya kimkakati.

Akihitimisha hotuba yake, Mheshimiwa Mavunde alisema Tanzania imejipanga kujenga sekta ya madini ya kisasa, thabiti na yenye ushindani wa kimataifa inayozingatia uwazi, uhakika na ushirikiano wa muda mrefu.

Alisema makubaliano hayo yanaashiria enzi mpya ya ushirikiano kati ya Serikali, wawekezaji na wananchi, yakionyesha kuwa uwekezaji, uzalendo na ukuaji wa uchumi vinaweza kwenda sambamba.

“Utajiri wa madini wa Tanzania lazima ugeuzwe kuwa ajira, viwanda, maarifa na matumaini kwa vizazi vijavyo,” alisema.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Lindi Jumbo, Andrew Cunningham, alisema utiaji saini wa makubaliano hayo ni ishara ya mafanikio ya safari ndefu ya maendeleo ya mradi huo pamoja na mwanzo wa hatua mpya ya ushirikiano na ukuaji wa sekta ya kinywe nchini Tanzania.

Bwana Cunningham alisema Mradi wa Lindi Jumbo ulianza zaidi ya miaka kumi iliyopita, huku shughuli za utafiti wa madini zikianza mwaka 2015 kwa lengo la kufungua fursa ya utajiri wa grafiti nchini Tanzania.

Alisema tangu wakati huo mradi huo umepitia hatua mbalimbali zikiwemo utafiti, tafiti za kitaalamu, upatikanaji wa fedha, ujenzi na uzalishaji hadi kufikia kuwa moja ya migodi bora ya kinywe duniani.

“Lindi Jumbo unakadiriwa kuwa na maisha ya mgodi ya miaka 24, huku ukiwa na uwezekano mkubwa wa kuongeza shughuli za uzalishaji hadi zaidi ya miaka 50 kutokana na utafiti unaoendelea,” alisema Bwana Cunningham. “Thamani ya mradi huu haipo tu katika muda wake mrefu wa uzalishaji, bali pia katika ubora mkubwa wa madini yake unaouweka katika nafasi nzuri katika soko la kimataifa la madini mkakati.”

Alisema kinywe imeendelea kuwa madini muhimu katika uchumi wa kisasa kutokana na matumizi yake katika shughuli za viwanda, teknolojia za kisasa na mifumo mipya ya nishati.

Kuhusu uzalishaji, mkurugenzi huyo alisema, mwaka 2025 mgodi huo ulisindika karibu tani kavu 170,000 za madini ghafi na kuzalisha tani 16,421 za kinywe yenye kiwango cha ubora kati ya asilimia 94 na 96 TGC.

Aliongeza kuwa mradi huo ulichimba zaidi ya tani 500,000 za mchanga na miamba katika kipindi hicho, huku oda za mauzo zilizothibitishwa zikizidi tani 27,800.

Bwana Cunningham pia alieleza mchango wa mradi huo kwa uchumi wa Tanzania, akisema kampuni ilitumia shilingi bilioni 57.5 kwa wazabuni wa ndani kati ya mwaka 2024 na 2025, ambapo asilimia 91 ya manunuzi yote yalielekezwa kwa kampuni za Kitanzania.

Aidha, kampuni hiyo ilichangia zaidi ya shilingi bilioni 11.3 kupitia mrabaha, kodi na malipo mbalimbali ya kisheria kwa Serikali.

Kwa mujibu wa Bwana Cunningham, mradi huo pamoja na wakandarasi wake unaajiri watu 280, ambapo zaidi ya asilimia 95 ni Watanzania, huku zaidi ya nusu ya wafanyakazi wakitoka vijiji vinavyozunguka Wilaya ya Ruangwa.

Pia alieleza juhudi za kampuni katika uwekezaji kwa jamii, akibainisha kuwa zaidi ya shilingi milioni 162 zimetengwa kwa ajili ya programu za uwajibikaji kwa jamii katika sekta za afya, elimu na maendeleo ya jamii.

Miongoni mwa miradi hiyo ni ujenzi wa zahanati katika Kijiji cha Namilema kwa lengo la kuboresha huduma muhimu za afya kwa wananchi wa maeneo yanayozunguka mradi huo.

Waziri wa Madini, Mheshimiwa Anthony Mavunde (wa pili kushoto), akishikana mikono na Mkurugenzi wa Lindi Jumbo, Andrew Cunningham, baada ya hafla ya utiaji saini wa makubaliano kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Lindi Jumbo Limited kuhusu ushiriki wa Serikali katika Mradi wa kinywe wa Lindi Jumbo kupitia kampuni ya ubia ya Ndovu Graphite Limited, iliyofanyika jana katika Kijiji cha Matambarale, Wilaya ya Ruangwa mkoani Lindi. Wanaoangalia kutoka kulia ni Mwakilishi kutoka Ofisi ya Msajili wa Hazina, Emmanuel Luvanda; Mwakilishi wa Gemcorp, William Binedell; na Mwanasheria na Katibu wa Kampuni ya Lindi Jumbo, Ephraim Mrawa.

Waziri wa Madini, Mheshimiwa Anthony Mavunde (wa pili kushoto), akiwa na, kutoka kushoto, Mkurugenzi wa Lindi Jumbo, Andrew Cunningham; Mwanasheria na Katibu wa Kampuni ya Lindi Jumbo, Ephraim Mrawa; pamoja na Mwakilishi wa Gemcorp, William Binedell, wakionesha hati za mikataba, baada ya utiaji saini wa makubaliano kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Lindi Jumbo Limited kuhusu ushiriki wa Serikali katika Mradi wa kinywe wa kampuni hiyo kupitia kampuni ya ubia ya Ndovu Graphite Limited, iliyofanyika jana katika Kijiji cha Matambarale, Wilaya ya Ruangwa mkoani Lindi.


Waziri wa Madini, Mheshimiwa Anthony Mavunde, akisaini nyaraka za makubaliano pamoja na Mkurugenzi wa Lindi Jumbo, Andrew Cunningham (wa tatu kulia), na Mwakilishi wa Gemcorp, William Binedell (wa pili kulia), wakati wa hafla rasmi ya utiaji saini wa makubaliano kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Lindi Jumbo Limited kuhusu ushiriki wa Serikali katika Mradi wa kinywe wa kampuni hiyo kupitia kampuni ya ubia ya Ndovu Graphite Limited, iliyofanyika jana katika Kijiji cha Matambarale, Wilaya ya Ruangwa mkoani Lindi. Kulia ni Mwanasheria na Katibu wa Kampuni ya Lindi Jumbo, Ephraim Mrawa.



Waziri wa Madini, Mheshimiwa Anthony Mavunde, akihutubia wakati wa hafla rasmi ya utiaji saini wa makubaliano kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Lindi Jumbo Limited kuhusu ushiriki wa Serikali katika Mradi wa kinywe wa kampuni hiyo kupitia kampuni ya ubia ya Ndovu Graphite Limited, iliyofanyika jana katika Kijiji cha Matambarale, Wilaya ya Ruangwa mkoani Lindi.
Mkurugenzi wa Lindi Jumbo, Andrew Cunningham, akitoa shukrani baada ya hafla ya utiaji saini wa makubaliano kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Lindi Jumbo Limited kuhusu ushiriki wa Serikali katika Mradi wa Kinywe wa kampuni hiyo kupitia kampuni ya ubia ya Ndovu Graphite Limited, iliyofanyika jana katika Kijiji cha Matambarale, Wilaya ya Ruangwa mkoani Lindi. Waziri wa Madini, Mheshimiwa Anthony Mavunde, alikuwa mgeni rasmi.


Waziri wa Madini, Mheshimiwa Anthony Mavunde (kushoto), akipokelewa na Mtendaji Mkuu wa Lindi Jumbo, Paul Lombar, kabla ya kuongoza hafla ya utiaji saini wa makubaliano kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Lindi Jumbo Limited kuhusu ushiriki wa Serikali katika Mradi wa kinywe wa kampuni hiyo kupitia kampuni ya ubia ya Ndovu Graphite Limited, iliyofanyika jana katika Kijiji cha Matambarale, Wilaya ya Ruangwa mkoani Lindi.


Waziri wa Madini, Mheshimiwa Anthony Mavunde (kushoto), akipokelewa na Mkurugenzi wa Lindi Jumbo, Andrew Cunningham, alipoenda kuwa mgeni rasmi katika hafla ya utiaji saini wa makubaliano kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Lindi Jumbo Limited kuhusu ushiriki wa Serikali katika Mradi wa kinywe wa Lindi Jumbo kupitia kampuni ya ubia ya Ndovu Graphite Limited, iliyofanyika jana katika Kijiji cha Matambarale, Wilaya ya Ruangwa mkoani Lindi. Wa pili kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Nachingwea na Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Mheshimiwa Mohamed Moyo.


Top News