Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb.), amekutana na kumuaga Balozi mteule wa Tanzania nchini Comoro, Mhe. Salim Othman Hamad, katika kikao kilichofanyika katika ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam.

Katika kikao hicho, Waziri Kombo amemtaka Balozi Hamad kutumia ipasavyo diplomasia ya uchumi ili kuimarisha mahusiano ya kibiashara na uwekezaji kati ya Tanzania na Comoro, pamoja na kukuza sekta ya utalii. Akisisitiza umuhimu wa kutumia nafasi hiyo kuibua fursa mpya za kiuchumi zitakazowanufaisha wananchi wa pande zote mbili.

Vilevile, Waziri Kombo amesisitiza umuhimu wa kuendeleza ushirikiano wa kidiplomasia uliopo kati ya Tanzania na Comoro, akihimiza uwakilishi madhubuti unaolenga kulinda na kukuza maslahi ya Taifa.

Kwa upande wake, Mhe. Hamad amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan, kwa imani na dhamana aliyompa ya kuiwakilisha nchi, na kuahidi kuitumikia Tanzania kwa weledi na uadilifu.

Kabla ya uteuzi wake, Mhe. Hamad alikuwa Mshauri wa Rais anayeshughulikia masuala ya siasa.







Baraza la Madiwani la Halmashauri ya Wilaya ya Geita limefanya mkutano wake wa kawaida wa robo ya tatu ya mwaka wa fedha 2025/2026, huku likiweka msisitizo katika kuimarisha ushirikiano na uwajibikaji ili kuharakisha maendeleo ya wananchi.

Mkutano huo uliofanyika leo Aprili 29, 2026, katika Ukumbi wa Mikutano wa Halmashauri uliopo Nzera, ulihusisha mjadala wa kina wa taarifa za maendeleo kutoka katika kata zote 37. Taarifa hizo zimebainisha hatua zilizofikiwa katika utekelezaji wa miradi pamoja na changamoto zinazohitaji ufumbuzi wa haraka.

Akizungumza katika mkutano huo, Mwakilishi wa Vyama Rafiki, Ndugu Ramadhan Sengerema, ameshauri baraza hilo kuhakikisha changamoto za miundombinu ya barabara zinatafutiwa ufumbuzi wa kudumu.

Amesema hatua hiyo ni muhimu katika kuchochea ukuaji wa mapato ya halmashauri na kuwarahisishia wananchi shughuli zao za kiuchumi.

Ndugu Sengerema amewahimiza madiwani kuendelea kufanya mikutano ya kisheria na wananchi ili kusikiliza kero zao, huku akisisitiza kufanya kazi kwa weledi na kushirikiana na wataalamu ili kuimarisha uaminifu kwa umma.

Kwa upande wake, Katibu wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Geita, Komredi Michael Msuya, amelipongeza baraza hilo kwa utendaji kazi wake. Hata hivyo, amesisitiza umuhimu wa kuelekeza nguvu katika sekta ya elimu, hususan katika utatuzi wa kero ya madawati na ujenzi wa miundombinu ya vyoo mashuleni.

Aidha, Komredi Msuya ametoa wito kwa halmashauri kuendelea kushirikiana na sekta binafsi kupitia mifumo ya uwajibikaji wa makampuni kwa jamii (CSR), ili kuongeza kasi ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo wilayani humo.

Akifunga mkutano huo, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Geita.

Mhe. Jumanne Misungwi, amewataka madiwani kusimamia kikamilifu ukamilishaji wa miradi kwa wakati na kuhakikisha ukusanyaji wa mapato unasimamiwa kwa uadilifu mkubwa.

Mhe. Misungwi amehitimisha kwa kusema kuwa ushirikiano wa dhati kati ya viongozi na wataalamu ndiyo msingi mkuu utakaowezesha halmashauri hiyo kufikia dhamira yake ya kuleta maendeleo ya kweli kwa wananchi wa Geita.





Bodi ya Utalii Tanzania (TTB), kupitia Mkurugenzi Mkuu wake, Ephraim Mafuru, imepokea ugeni maalum kutoka Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH) ukiongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wa hospitali hiyo, Prof. Abel Makubi, kwa lengo la kuimarisha ushirikiano katika kukuza utalii wa matibabu nchini Tanzania na kushiriki katika Maadhimisho ya Miaka 10, tarehe 15 July 2026 ambapo pia Hospitali itakuwa ianzindua mfuko wa kusaidia huduma za Upandikizaji Uloto kwa Watoto na Upandikizaji Figo. 

Katika kikao hicho, taasisi hizo mbili zimejadili maeneo mbalimbali ya ushirikiano na kukubaliana kuendelea kuhamasisha utalii wa Matibabu kama moja ya mazao ya kipekee ya utalii nchini. Hatua hiyo inakuja wakati Hospitali ya Benjamin Mkapa ikiendelea kujipambanua kwa kutoa huduma za kibingwa na ubobezi wa hali ya juu, na kuifanya kuwa miongoni mwa hospitali bora za rufaa katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.

Akizungumza katika kikao hicho, Mafuru amesema Bodi ya Utalii imevutiwa sana na huduma sita za kibingwa zinazotolewa na hospitali hiyo, huku huduma mbili zikiwa za kipekee zaidi katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.

“Ni jambo la kujivunia Hospitali ya Benjamin Mkapa kuwa hospitali pekee Afrika Mashariki na Kati yenye utaalamu wa kupandikiza uloto kwa watoto waliozaliwa na selimundu (Sickle Cell), lakini pia huduma ya upandikizaji figo,” amesema Mafuru.

Ameeleza kuwa upekee wa hospitali hiyo unaweza kuinua taswira nzuri ya Tanzania katika sekta ya utalii wa tiba, sambamba na kuboresha maisha ya Watanzania kwa kuwapatia huduma za kibingwa ndani ya nchi badala ya kusafiri nje kutafuta matibabu.

Mafuru pia ametoa wito kwa wadau wote wa sekta ya utalii nchini kushiriki harambee ya kuanzisha mfuko maalum wa kusaidia matibabu ya wagonjwa wa selimundu na figo kwa wananchi wasio na uwezo. Harambee hiyo inatarajiwa kufanyika Julai 15, 2026, sambamba na maadhimisho ya miaka kumi tangu kuanzishwa kwa Hospitali ya Benjamin Mkapa.

Kwa upande wake, Prof. Makubi ameahidi kushirikiana kikamilifu na Bodi ya Utalii Tanzania katika kukuza zao hili la utalii wa tiba nchini, akisisitiza kuwa taasisi zote mbili zipo chini ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayoongozwa na Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan.

Amesema kuimarishwa kwa utalii wa tiba kutaiwezesha Tanzania kujijengea nafasi kubwa zaidi kama kitovu cha huduma za afya za kibingwa katika ukanda wa Afrika, huku pia ikichangia ukuaji wa uchumi wa taifa.

Ushirikiano huu unaendelea kufungua ukurasa mpya wa kuitangaza Tanzania si tu kama kivutio cha wanyamapori, fukwe na urithi wa utamaduni, bali pia kama kitovu cha huduma za afya za ubora wa kimataifa.






Na: Mohammed Hammie 

Wakati masuala ya hedhi yakiendelea kuzungumzwa kwa sauti ya chini katika jamii nyingi, kijana mmoja kutoka kijiji cha Lipwidi mkoani Mtwara ameamua kuvunja ukimya huo, na cha kushangaza zaidi, yeye ni mwanaume.

Makungu Mrope (24), anayejulikana kwa jina la utani “Kaka wa Hedhi”, anajitolea kutoa elimu ya hedhi salama kwa wasichana, wanawake na hata wanaume katika jamii yake. Kupitia juhudi zake, anabadilisha mtazamo uliokita mizizi kwamba hedhi ni suala la siri linalowahusu wanawake pekee.

Safari ya Mrope ilianza tangu utotoni, baada ya kushuhudia tukio lililomuacha na maswali mengi. Dada yake alipata hedhi akiwa shuleni wakati wa mapumziko na kukumbana na dhihaka kutoka kwa wanafunzi wenzake.

“Walianza kumzomea na kuimba kuwa amechinja kuku. Ilikuwa aibu kubwa sana,” anasimulia Mrope.

Anasema wakati huo hakuelewa kilichotokea hadi alipofuatilia baada ya siku chache. Kilichomuumiza zaidi ni kuona dada yake akizuiwa kwenda shule kwa wiki nzima kutokana na tukio hilo.

“Tukio lile liliniumiza sana. Ndipo nikaweka nia kwamba nitakapokuwa mkubwa nitaelimisha kuhusu hedhi salama ili wasichana wasipitie mateso kama yale,” anasema.

Baada ya kushindwa kuendelea na masomo ya juu ya sekondari, Mrope aligeukia kujielimisha kupitia zahanati ya kijiji na machapisho ya Wizara ya Afya. Hatimaye alianza kutoa elimu hiyo kwa jamii yake.

Juhudi zake zilitambuliwa na uongozi wa kijiji cha Lipwidi, uliompa kibali cha kuendesha shughuli zake rasmi za uelimishaji. Tangu hapo, amekuwa akitembelea shule mbalimbali kutoa elimu ya hedhi salama.

Kila asubuhi, Mrope huanza siku yake kwa kutembelea shule ya sekondari aliyosoma, ambapo hupata dakika 30 wakati wa gwaride la asubuhi kuzungumza na wanafunzi. Katika vipindi hivyo, hutoa elimu na kujibu maswali mbalimbali kutoka kwa wanafunzi.

“Sifanyi kazi hii peke yangu. Mara nyingi nashirikiana na wataalamu wa afya kutoka zahanati ya kijiji,” anasema.

Mbali na shughuli za uelimishaji, Mrope pia anajishughulisha na biashara ya kuuza nguo za kiume. Hata hivyo, dukani kwake pia hupatikana taulo za kike (pedi), jambo lisilo la kawaida kwa wafanyabiashara wengi wa aina hiyo.

Anasema kila mteja anayenunua bidhaa hiyo hupata pia elimu ya matumizi sahihi na umuhimu wa usafi wa hedhi.

Mrope anaamini kuwa wanaume wana nafasi muhimu katika kubadili mtazamo wa jamii kuhusu hedhi.

“Ninapenda kuwaelimisha wanaume wenzangu kuhusu umuhimu wa hedhi kwa wanawake na wasichana. Wengi wameanza kubadilika,” anasema.

Anaongeza kuwa ushiriki wa wanaume unaweza kusaidia kuondoa unyanyapaa, kuboresha afya ya uzazi, na kuongeza uelewa sahihi kuhusu hedhi kama suala la kiafya badala ya aibu au siri.

Wakati dunia ikiadhimisha Siku ya Hedhi kila mwaka tarehe 28 Mei, jitihada za Mrope zinaakisi lengo la siku hiyo, kuongeza uelewa, kuondoa unyanyapaa, na kuhakikisha upatikanaji wa vifaa salama vya hedhi kwa wasichana na wanawake.

Kwa kupitia kazi yake, “Kaka wa Hedhi” anaendelea kuwa sauti muhimu ya mabadiliko katika jamii, akionesha kuwa elimu ya hedhi salama ni jukumu la kila mtu, bila kujali jinsia. 



 

Na: Jawadu Kinyobwa

Tanzania imezidi kujiimarisha kama kitovu cha mafunzo utawala bora barani Afrika baada ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete, kupokea ujumbe wa watu 25 kutoka nchini Somalia kwa ajili ya programu maalumu ya mafunzo ya kuendesha shughuli za utumishi wa umma kwa ufanisi.

Akizungumza mara baada ya kuwakaribisha wajumbe hao Aprili 28 , Mhe. Kikwete ameeleza kuwa ujio huo ni kielelezo cha imani ambayo mataifa mengine wanayo kwa Tanzania kama nchi ya mfano katika kuimarisha amani, utulivu na maendeleo ya kiutawala. 

Amesema lengo kuu la ugeni huo ni kujifunza namna mifumo ya utumishi wa umma nchini inavyofanya kazi, ikiwemo usimamizi wa rasilimali watu na namna utumishi huo unavyoweza kujibu kero za wananchi kwa haraka na usahihi.

Waziri Kikwete amesisitiza kuwa Watanzania wapaswa kujua kwamba "wamekalia dhahabu" kutokana na mabadiliko makubwa ya kimfumo yaliyofanyika, hususan katika kipindi cha Serikali ya Awamu ya Sita inayowezesha wananchi kuwasiliana moja kwa moja na serikali yao. 

Amebainisha kuwa matumizi ya teknolojia (Digitalization) yamerahisisha huduma ambapo kwa sasa mtumishi wa umma hahitaji kusafiri kutoka mkoani kwenda Dodoma kufuata huduma, bali anaweza kupata mahitaji yake, ikiwemo maombi ya mikopo na mawasiliano na viongozi, kupitia mifumo ya kidijitali iliyowekwa.

Kwa upande wake, Kaimu Katibu Mkuu ambaye pia Naibu Katibu Mkuu wa ofisi hiyo, Bw. Xavier Daudi, amefafanua kuwa wajumbe hao watapitishwa kwenye maeneo muhimu ya kiutendaji ikiwemo muundo wa serikali, mifumo ya Serikali Mtandao (e-Government), na mbinu za kisasa za utunzaji wa nyaraka. 

Amesema upekee wa mifumo ya Tanzania na miundombinu yake ya kisasa ya kiutendaji ndivyo vinavyovutia nchi nyingi za Afrika Mashariki na kwingineko kuja kujifunza.

Awali akizungumza Mkuu wa Chuo na Mtendaji Mkuu wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC), Ernest Mabonesho, ambaye ndiye mratibu wa programu hiyo, amebainisha kuwa mafunzo hayo ni matokeo ya makubaliano yaliyofikiwa mwaka 2025 kupitia Wizara ya Mambo ya Nje. 

Amesema zoezi hilo ni muendelezo wa ushirikiano wa kihistoria kati ya Tanzania na Somalia, wenye lengo la kujenga kuwezesha serikali kufanya kazi kwa tija na kwa manufaa ya mataifa yote mawili.

Naye, mmoja wa washiriki wa mafunzo hayo kutoka Somalia, Ayan Andullahi ameeleza kuwa kupitia mafunzo hayo amejifunza kwa kina kuhusu namna Tanzania ilivyofanikiwa kujenga mifumo madhubuti ya utumishi wa umma inayozingatia uwajibikaji, uwazi na utoaji wa huduma ufanisi na kwa wakati.

Amesisitiza kuwa, uzoefu alioupata, hususan katika matumizi ya mifumo ya kidijitali na uratibu wa rasilimali watu utakuwa chachu ya mageuzi katika taasisi yao pindi watakaporejea nchini Somalia









 

Na Munir Shemweta

Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi imempokea mjumbe maalum kutoka Shirika la Umoja wa Mataifa la Makazi Duniani (UN-Habitat) kwa ajili ya kukagua maandalizi ya kufunguliwa kwa ofisi za shirika hilo nchini.

Mjumbe huyo maalum, Bw. Grace Lubale, yupo nchini kwa ziara ya siku tatu inayolenga kutembelea na kukagua ofisi zilizotolewa na Serikali ya Tanzania kwa UN-Habitat, ambazo zipo katika jengo la Wizara hiyo lililopo Mji wa Serikali Mtumba, jijini Dodoma.

Ziara hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa makubaliano ya ushirikiano yaliyosainiwa tarehe 7 Juni 2023 kati ya Serikali ya Tanzania na UN-Habitat, yakilenga kuimarisha ushirikiano katika sekta ya makazi na maendeleo ya miji.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo tarehe 28 April 2026 jijini Dodoma, Mkurugenzi wa Maendeleo ya Makazi kutoka Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Bw. Deogratius Kalimenze, amesema Serikali imejipanga kikamilifu kuhakikisha ofisi hiyo inaanza kazi kwa ufanisi, ikiwa ni pamoja na kutoa vitendea kazi na wataalam wanne watakaosaidia uendeshaji wake.

‘’Serikali ina matarajio makubwa kutokana na uwepo wa ofisi hii, hususan katika kuimarisha juhudi za kushughulikia changamoto mbalimbali katika sekta ya makazi, ikiwemo maendeleo ya miji, matumizi ya nishati jadidifu, ustahimilivu wa miji, pamoja na uboreshaji wa makazi yasiyopangwa’’. ameeleza Bw. Kalimenze.

Kwa upande wake, Bw. Grace Lubale amesema UN-Habitat inaendelea kushirikiana kwa karibu na Serikali ya Tanzania ili kuhakikisha malengo ya ushirikiano huo yanatekelezwa kwa kuzingatia viwango vya kimataifa vya shirika hilo.

‘’Kupitia ushirikiano huu, maeneo yatakayopatiwa kipaumbele ni pamoja na uboreshaji wa makazi, ujenzi wa nyumba za gharama nafuu pamoja na nishati safi katika majengo’’. amesema,

Ushirikiano kati ya pande hizo mbili pia unalenga kuwezesha upatikanaji wa wadau wa maendeleo na mifumo ya Umoja wa Mataifa katika kusaidia utekelezaji wa miradi ya makazi, pamoja na kuanzisha mifumo madhubuti ya ufuatiliaji wa utekelezaji wa malengo ya maendeleo endelevu, hususan lengo namba 11 linalohusu miji na makazi endelevu.

Hatua ya kufunguliwa kwa ofisi ya UN-Habitat nchini Tanzania inatarajiwa kuwa chachu ya kuimarisha maendeleo ya sekta ya makazi na miji, na kuongeza ushirikiano wa kimataifa katika kutatua changamoto za makazi nchini.

 Mkurugenzi wa Maendeleo ya Makazi kutoka Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Bw. Deogratius Kalimenze (katikati) akimsikiliza Mjumbe Maalum Shirika la Umoja wa Mataifa la Makazi Duniani (UN-Habitat) Bw. Grace Lubale (kushoto) wakati wa kikao kichofanyika katika mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma. Kulia ni Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Maendeleo ya Makazi Bw. Nicholaus Mwakasege

Maafisa wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi wakiwa katika kikao na Mjumbe Maalum Shirika la Umoja wa Mataifa la Makazi Duniani (UN-Habitat) Bw. Grace Lubale wakati wa kikao kilichofanyika makao makuu ya wizara Mtumba jijini Dodoma.
Mkurugenzi wa Maendeleo ya Makazi kutoka Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Bw. Deogratius Kalimenze (wa pili kushoto) na Mjumbe maalum Shirika la Umoja wa Mataifa la Makazi Duniani (UN-Habitat) Bw. Grace Lubale (wa pili kulia) wakiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya maafisa wa Wizara ya Ardhi mara baada ya kukagua ofisi ambazo UN-Habitat inatarajia kuzifungua jijini Dodoma. (PICHA NA WIZARA YA ARDHI)





Mwezi Aprili 2026 unabaki kuwa kipindi kinachoakisi uongozi wa vitendo uongozi unaosikiliza, unaouliza maswali sahihi na unaotafuta majibu yenye tija kwa wananchi, ni mwezi ambao umeonesha kwa dhahiri namna Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Dodoma, Dkt. Neema Peter Majule, anavyobeba dhamana ya uwakilishi kwa uzito na weledi.

Ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Majule ameendelea kuwa sauti ya wale wanaotazama matumaini yao kupitia viongozi wanawake, vijana na watu wenye ulemavu, Kwa hoja zenye mwelekeo wa maendeleo, alihoji ni lini Serikali itawekeza kikamilifu katika ujenzi wa viwanda vitakavyofungua milango ya ajira, akisisitiza kuwa mikopo midogo midogo, ingawa ni muhimu, haiwezi peke yake kubadili kwa kiwango kikubwa maisha ya watu.

Majibu ya Serikali yalieleza mwelekeo wa hatua kwa hatua kuwa baadhi ya wanufaika wa mikopo hiyo wameweza kukuza biashara zao, kurejesha mikopo na hatimaye kufikia hatua ya kupata mitaji mikubwa iliyowezesha kuanzishwa kwa viwanda vidogo, hii ni picha ya mafanikio yanayokua taratibu, lakini pia inaacha nafasi ya kujiuliza: je, kasi inaweza kuongezwa zaidi?

Katika kuonesha kuwa uongozi si kauli pekee bali ni matokeo yanayoonekana, tarehe 14 Aprili 2026, Dkt. Majule aliratibu utoaji wa mikopo ya shilingi bilioni moja kwa wanawake na vijana wajasiriamali wa Mkoa wa Dodoma kwa kushirikiana na Benki ya CRDB, Hapa ndipo nadharia inakutana na uhalisia ndoto za wajasiriamali zikipewa mtaji, na juhudi zao kupewa mwelekeo mpya wa ukuaji.

Kwenye sekta ya miundombinu, alielekeza mjadala kwenye changamoto ya mvua zinazosababisha uharibifu wa barabara Dodoma, kwa mtazamo wa mbele, aliitaka Serikali kuweka mifumo ya kudumu ya mifereji ili kulinda uwekezaji huo muhimu.

Serikali ilijibu kwa kueleza kuwa inaboresha usanifu wa barabara zote mpya ili ziwe na mifereji ya kudumu ya maji, hatua inayolenga kuongeza uimara na maisha ya miundombinu hiyo, hii inaonesha jinsi hoja zinavyoweza kuwa chachu ya maboresho ya sera na utekelezaji.

Aidha, alifuatilia kwa karibu ujenzi wa barabara ya Kongwa Junction hadi Mpwapwa na Kibakwe ni barabara ambayo kwa muda mrefu imekuwa kilio cha wananchi, swali lake lilikuwa la moja kwa moja ni lini barabara hiyo itajengwa kwa kiwango cha lami?

Majibu ya Serikali yalieleza kuwa utekelezaji wake utategemea vipaumbele vilivyopo, huku miradi yenye mikataba tayari ikipewa kipaumbele. Ni jibu linaloonesha uhalisia wa upangaji wa miradi ya kitaifa, lakini pia linatoa mwanga wa matarajio ya utekelezaji wake hapo baadaye.

Katika eneo la haki na ustawi wa jamii, tarehe 24 Aprili 2026, Dkt. Majule aligusa moyo wa wengi kwa kuzungumzia ucheleweshaji wa vyeti vya vifo kutoka RITA, Hapa hakuzungumza kwa takwimu pekee bali kwa uhalisia wa maisha ya yatima wanaokwama kielimu na wajane wanaochelewa kupata haki zao za msingi.

Alisisitiza kuwa huduma hizi hazipaswi kucheleweshwa, na akaishauri Serikali kuongeza ufanisi katika taasisi hiyo, Ingawa majibu ya kina hayakuainishwa wazi, hoja yake ilibeba uzito wa kuamsha mjadala mpana juu ya uwajibikaji wa taasisi za umma.

Katika upande wa mafanikio, aliipongeza Serikali kwa kampeni ya Mama Samia Legal Aid Campaign, akibainisha mchango wake katika kusogeza huduma za kisheria kwa wananchi wa kawaida. Lakini kama ilivyo hulka ya uongozi makini, hakusimama kwenye pongezi alipendekeza kuanzishwa kwa mfuko maalum wa kusaidia gharama za usafiri na mahitaji ya msingi kwa wananchi wanaofuatilia kesi zao, pamoja na kuhimiza kasi ya usikilizwaji wa kesi mahakamani.

Nje ya ukumbi wa Bunge, Dkt. Majule aliendelea kuishi kile anachokiamini ushiriki wake katika matukio kama Bunge Marathon umeonesha kuwa uongozi hauishii kwenye hotuba, bali unahusisha uwepo wa karibu na jamii, kuhamasisha afya, mshikamano na umoja.

Kwa ujumla, Aprili 2026 si tu mwezi wa matukio, bali ni kioo kinachoonesha aina ya uongozi unaohitajika, uongozi unaounganisha sauti za wananchi na mifumo ya maamuzi, unaosukuma majibu kutoka kwa mamlaka, na unaoweka mbele maslahi ya watu.

Dkt. Neema Peter Majule anajitokeza kama kiongozi wa aina hiyo anayesikiliza kwa makini, anauliza kwa ujasiri, na anafuatilia kwa uthabiti hadi majibu yageuke kuwa matendo ni uongozi unaoleta matumaini unaojenga kesho iliyo bora.


Na Janeth Raphael- MichuziTv -Dodoma 

Tanzania imepata heshima kubwa ya kuwa mwenyeji wa Mkutano Mkuu wa Pili wa Mwaka wa Jumuiya za Wataalamu wa Usimamizi wa Rasilimaliwatu na Utawala Bora barani Afrika, tukio litakalowakutanisha wataalamu kutoka mataifa mbalimbali kwa lengo la kubadilishana uzoefu, kujengeana uwezo na kuimarisha mifumo ya utumishi wa umma katika bara la Afrika.

Mkutano huo mkubwa umepangwa kufanyika kuanzia tarehe 5 hadi 8 Mei, 2026 katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC), ambapo Tanzania itawakilishwa na taasisi zote zilizo chini ya Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Aprili 29, 2026 jijini Dodoma, Mwenyekiti wa African Association for Public Administration and Management (AAPAM) Tanzania Chapter, Leila Mavika, amesema maandalizi ya mkutano huo yamekamilika kwa kiwango kikubwa na unatarajiwa kuwa na matokeo chanya kwa maendeleo ya utawala bora barani Afrika.

Mavika alieleza kuwa mkutano huo umeandaliwa na AAPAM, taasisi inayojumuisha nchi zote wanachama barani Afrika kupitia matawi yake ya kitaifa, ambapo Tanzania ina AAPAM Tanzania Chapter inayoratibiwa chini ya Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma kama mlezi wa taasisi hiyo nchini.

Ameongeza kuwa mkutano huo wa pili wa mwaka utakuwa jukwaa muhimu la kitaaluma litakalowakutanisha wataalamu wa utawala wa umma, usimamizi wa rasilimaliwatu na utawala bora kutoka nchi mbalimbali za Afrika, kwa lengo la kujadili changamoto, fursa na mbinu bora za kuboresha utendaji wa sekta ya umma.

Aidha, Mavika amebainisha kuwa mkutano huo utashirikisha pia Jumuiya ya Wataalamu wa Utawala wa Umma na Usimamizi wa Rasilimaliwatu Tanzania (TAPAHR) pamoja na Mtandao wa Mameneja wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu Tanzania (TPS-HRMnet), katika kuimarisha ushirikiano wa kitaaluma na kikanda.

Katika hatua nyingine, ametoa wito kwa waajiri wote katika Wizara, Tawala za Mikoa, Mamlaka za Serikali za Mitaa, Wakala za Serikali, Mashirika ya Umma, Vyuo Vikuu na Vyuo vya Kati kuhakikisha wanawapatia wataalamu wao wa utumishi wa umma nafasi ya kushiriki kikamilifu katika mkutano huo.

Amesema ushiriki huo utawasaidia kuongeza ujuzi, kubadilishana uzoefu na kuimarisha utendaji kazi katika maeneo yao ya kazi, hatua ambayo itachangia kwa kiasi kikubwa kuboresha huduma kwa wananchi.

Mkutano huo unatarajiwa kuwa moja ya matukio makubwa ya kikanda katika mwaka 2026, ukiweka Tanzania katika ramani ya uongozi wa mijadala ya utawala bora na maendeleo ya rasilimaliwatu barani Afrika.




 

Waziri wa Elimu,Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda,akizungumza wakati akifungua  Mkutano wa 37 wa Baraza la Wafanyakazi wa wizara hiyo uliofanyika leo Aprili 29,2029 jijini Dodoma.

Waziri wa Elimu,Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda,akizungumza wakati akifungua  Mkutano wa 37 wa Baraza la Wafanyakazi wa wizara hiyo uliofanyika leo Aprili 29,2029 jijini Dodoma.

Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Nombo,akizungumza wakati wa   Mkutano wa 37 wa Baraza la Wafanyakazi wa wizara hiyo uliofanyika leo Aprili 29,2029 jijini Dodoma.

Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Nombo,akizungumza wakati wa   Mkutano wa 37 wa Baraza la Wafanyakazi wa wizara hiyo uliofanyika leo Aprili 29,2029 jijini Dodoma.

Sehemu ya washiriki wakimsikiliza Waziri wa Elimu,Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda (hayupo pichani) wakati wa  Mkutano wa 37 wa Baraza la Wafanyakazi wa wizara hiyo uliofanyika leo Aprili 29,2029 jijini Dodoma.

Waziri wa Elimu,Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda,akiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kufungua   Mkutano wa 37 wa Baraza la Wafanyakazi wa wizara hiyo uliofanyika leo Aprili 29,2029 jijini Dodoma.

Waziri wa Elimu,Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda,akiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kufungua   Mkutano wa 37 wa Baraza la Wafanyakazi wa wizara hiyo uliofanyika leo Aprili 29,2029 jijini Dodoma.

....

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda, amesema utekelezaji wa mageuzi ya elimu unaoendelea nchini ni sehemu ya dhamira thabiti ya Serikali ya Awamu ya Sita ya kuhakikisha vijana wanapatiwa ujuzi, maarifa na uwezo unaowawezesha kushiriki kikamilifu katika uchumi wa taifa.

Ameyasema hayo leo  Aprili 29, 2026 katika Mkutano wa 37 wa Baraza la Wafanyakazi wa wizara hiyo, Prof. Mkenda amesisitiza kuwa sekta ya elimu inabeba wajibu mkubwa katika maendeleo ya nchi na kwamba, wajibu wa Wizara ni kuhakikisha mipango yote inatekelezwa kwa ufanisi na kwa kasi.

Waziri Mkenda ameongeza kuwa kuanzishwa kwa Wizara maalum ya maendeleo ya vijana ni uthibitisho wa umuhimu wa kundi hilo katika maendeleo ya taifa na kuwa elimu ya ufundi kupitia VETA, ni msingi wa kuwaandaa vijana kuzalisha na kushiriki katika uchumi wa kisasa.  "Utekelezaji wa elimu ya miaka 10 ya lazima na uimarishaji wa shule za Sekondari na shule za amali unatekelezwa kwa ushirikiano wa karibu na Ofisi ya Rais – TAMISEMI, na hata sekta binafsi hasa katika kuhakikisha upatikanaji wa shule karibu na makazi ya wananchi na ununuzi wa vifaa vya kisasa kwa ajili ya mafunzo ya ufundi."amesema Prof. Mkenda Katika kuhimiza ubunifu na uwajibikaji, Prof. Mkenda amewataka watumishi wa Wizara kuendeleza kasi ya utendaji na kuhakikisha wananchi wanaendelea kupata taarifa kuhusu utekelezaji na mafanikio ya serikali katika maeneo ya sekta ya elimu, sayansi, teknolojia na ubunifu.

Kwa upande wake Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Nombo,amesema Serikali inaendelea kuimarisha usimamizi wa ajira na rasilimaliwatu kwa kuzingatia malengo na maono ya Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan hususan katika utekelezaji wa Kifungu cha 73 cha Sheria ya Ajira kinachohusu uhusiano kazini.

Prof. Nombo amesema kuwa kupitia mkutano huo, wajumbe watapitia mpango na bajeti ya wizara pamoja na masuala ya utawala na usimamizi wa rasilimali watu pamoja na kujadili masuala mbalimbali yanayolenga kuboresha afya na usalama mahali pa kazi. Prof. Nombo amesisitiza kuwa mshikamano na ushirikiano miongoni mwa wafanyakazi ni nguzo muhimu ya kufanikisha ubora na uaminifu katika utendaji kazi,  "Dhamira ya Wizara ni kuona watumishi wanafanya kazi kwa bidii, kwa uadilifu na kwa kuzingatia maadili ya utumishi wa umma ili kuendeleza mageuzi yanayoendelea katika elimu."amesema Prof. Nombo Aidha, amewashukuru wajumbe wa Baraza hilo kwa ushirikiano wao na amewataka kuendekeza juhudi za kuimarisha mifumo ya usimamizi ndani ya Wizara.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo na Waziri wa Mambo ya Nje wa Belarus, Maxim Ryzhenkov wakisaini mkataba wa makubaliano ya kushirikiana katika Uchumi, mkataba huo umesainiwa leo Aprili 29, 2026 jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo na Waziri wa Mambo ya Nje wa Belarus, Maxim Ryzhenkov wakionesha mkataba wa makubaliano ya kushirikiana katika Uchumi, mkataba huo ambao wameusaini leo Aprili 29, 2026 jijini Dar es Salaam.


SERIKALI ya Tanzania na Belarus zimesaini mkataba wa makubaliano (MoU) ya kuanzisha kamati maalumu ya ushirikiano wa kiuchumi na kibiashara, hatua inayolenga kuratibu mahusiano yao na kufungua ukurasa mpya wa maendeleo.

Makubaliano hayo yamesainiwa leo Aprili 29 2026 jijini Dar es Salaam na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo pamoja na Waziri wa Mambo ya Nje wa Belarus, Maxim Ryzhenkov.

Akizungumza baada ya kusaini ushirikiano huo, Profesa Kitila anasema hatua hiyo inalenga kufufua mahusiano kati ya Tanzania na Belarus ambayo yanasimama kwa takribani miaka 30 iliyopita.

Amesisitiza kuwa makubaliano hayo yanafungua fursa za uwekezaji kutoka Belarus katika sekta mbalimbali zikiwemo kilimo, viwanda na biashara, hali inayotarajiwa kuongeza ajira na mapato ya taifa.

Aidha, amesema ushirikiano huo utaisaidia Tanzania katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya 2050 kwa kuvutia wawekezaji wapya, kuleta teknolojia za kisasa na kuongeza ushindani wa uchumi.

Katika hatua nyingine, Profesa Mkumbo amebainisha kuwa kuna mpango wa kupeleka vijana nchini Belarus ili kujifunza teknolojia mbalimbali, hususani zitakazosaidia kuboresha sekta ya kilimo.

Kwa upande wake, Ryzhenkov amesema anafuraha sana kwamba wamesaini makubaliano ya kuanzisha Kamati ya Pamoja ya Biashara na Uchumi na hicho kitakuwa chombo muhimu kwa mahusiano yao.

Amesema wanaitazama Tanzania kama mshirika muhimu na lango lao kuu la ukuaji katika ukanda huu, hivyo wapo tayari kuwekeza katika miradi ambayo haitachochea tu biashara kati ya nchi zao, bali pia kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha kimkakati kwa biashara yetu barani Afrika.

“Tunaitazama Tanzania kama mshirika muhimu na lango letu kuu la ukuaji katika ukanda huu. Tuko tayari kuwekeza katika miradi itakayoiwezesha Tanzania kuwa kitovu cha kimkakati cha biashara barani Afrika,”amesema Ryzhenkov.

Amesema katika ziara yao, walitembelea maeneo kadhaa ya kuvutia, ikiwemo maeneo ya usindikaji wa bidhaa za mauzo ya nje na kwa sasa wanatafakari namna bora ya kushiriki kikamilifu katika mifumo hiyo.

Pia amesema kampuni kadhaa za Belarus zimeonyesha nia ya kutumia maeneo hayo hususani kuna nia ya kuanzisha kituo cha kikanda cha mbolea na bidhaa nyingine kitakachohudumia si Tanzania pekee bali pia ukanda mpana wa Afrika Mashariki.

Ryzhenkov amesema makubaliano mengine kadhaa ya msingi yako mezani kwa sasa lakini hadi kufikia ziara ya Waziri Mkuu wao Oktoba, mwaka huu watakuw awamekamilisha, makubaliano hayo yakiwemo ulizi wa uwekezaji na ushirikia no katika huduma za forodha.

Amesema mbali na biashara anatarajia kuona ushirikiano wao ukitanuka hadi kwenye masuala ya kibinadamu, mazungumzo ya kisiasa na mambo ya nje, yeye na wenzake na wamejizatiti kurahisisha mahusiano hayo na kuimarisha ushirikiano wa biashara kwa biashara pamoja na watu kwa watu

Pia amesema wako tayari kuanzisha mawasiliano ya moja kwa moja kati ya vyuo vikuu vya nchi zote na vituo vya utafiti ili kukuza miradi ya pamoja ya utafiti yenye manufaa kwa pande zote na kuleta karibu zaidi jumuiya za kisayansi za nchi zao.








Matukio mbalimbali.


Top News