Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akimjulia hali Sheikh Rashid Hamad Othman, Kaka mkubwa wa Mwenyekiti wa Taifa wa Chama cha ACT Wazalendo, Mhe. Othman Masoud Othman, anayepatiwa matibabu katika Hospitali ya Aga Khan Jijini Dar es Salaam. Akiwa hospitalini hapo Mhe. Rais Dkt. Samia pia alijulishwa kuhusu kuwepo kwa Mchezaji wa Timu ya Yanga Pacome Zouzoua katika chumba jirani, ambapo alipata muda wa kumtembelea na kumpa pole kufuatia majeraha aliyopata katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC dhidi ya JKT Tanzania katika Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo hivi karibuni.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema kuna umuhimu mkubwa kwa nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki kuimarisha ushirikiano katika nyanja ya diplomasia ya uchumi, biashara na uwekezaji.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, tarehe 06 Julai 2026, alipokutana na Balozi mpya wa Tanzania nchini Uganda, Mhe. Balozi Meja Jenerali Marco Elisha Gaguti, aliyefika Ikulu Zanzibar kwa ajili ya kuaga kabla ya kuelekea katika kituo chake cha kazi.

Rais Dkt. Mwinyi amesema ni wakati muafaka kwa nchi za Afrika Mashariki kuendelea kuimarisha ushirikiano wa kibiashara na uwekezaji, kwa lengo la kunufaika na fursa mbalimbali za kiuchumi zilizopo katika mataifa hayo.

Ameeleza kuwa uhusiano mzuri baina ya mataifa hayo ni msingi muhimu wa kukuza uchumi na kuimarisha ustawi wa wananchi.

Aidha, Rais Dkt. Mwinyi amemsisitiza Balozi Marco kutumia nafasi yake kuzitangaza fursa za uwekezaji na vivutio vya utalii vilivyopo Tanzania, ikiwemo Zanzibar, nchini Uganda, hususan kwa makampuni, wafanyabiashara na wawekezaji wakubwa, ili waweze kuja kuwekeza nchini.

Rais Dkt. Mwinyi amemhakikishia Balozi Marco ushirikiano mkubwa katika utekelezaji wa majukumu yake mapya ya kibalozi, huku akimshauri kuchukua juhudi maalum za kuwashawishi na kuwaunganisha wafanyabiashara na wawekezaji wa Uganda kutumia fursa zilizopo kuwekeza Tanzania.

Kwa upande wake, Mhe. Balozi Meja Jenerali Marco Elisha Gaguti amemhakikishia Rais Dkt. Mwinyi kuwa atafanya kila linalowezekana kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi, kwa kuzingatia miongozo na maelekezo aliyopokea, sambamba na kuendeleza kimkakati diplomasia ya uchumi baina ya Tanzania na Uganda.











Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

OFISI ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma imesema haina tatizo na viongozi wa umma wenye utajiri, ilimradi mali walizonazo zimepatikana kwa njia halali bila kutumia vibaya madaraka yao au kufanya biashara zinazokinzana na nafasi wanazoshikilia serikalini.

Hayo ameyasema Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini wa Ofisi hiyo, Honoratus Ishengoma, wakati akizungumza na wananchi waliotembelea banda la Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.

Ishengoma alisema viongozi wa umma wanatakiwa kuzingatia masharti ya kimaadili yaliyowekwa na sheria, ikiwemo wajibu wa kutangaza mali na madeni yao pamoja na kueleza vyanzo vya mapato yao ili kuhakikisha uwazi na uwajibikaji katika utumishi wa umma.

Amesema kuwa lengo la ushiriki wa Sekretarieti katika maonesho hayo ni kutoa elimu kwa wananchi kuhusu majukumu ya taasisi hiyo, maadili yanayopaswa kuzingatiwa na viongozi wa umma pamoja na umuhimu wa kuzingatia miiko ya uongozi katika utendaji wa kila siku.

Aidha, alisema sheria haiwazuii viongozi wa umma kufanya biashara au shughuli nyingine za kiuchumi, mradi shughuli hizo hazisababishi mgongano wa maslahi na majukumu yao ya kikazi au kutumia nafasi za uongozi kujinufaisha binafsi.

Aliwahimiza wananchi kutembelea banda la Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma katika maonesho ya Sabasaba ili kupata elimu kuhusu maadili ya viongozi, wajibu wa viongozi kutangaza mali zao na nafasi ya wananchi katika kuimarisha uwajibikaji na utawala bora nchini.
Na Mwandishi Wetu
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imesema matumizi ya teknolojia katika sekta ya ushirika yataongeza uwazi, uwajibikaji na ushirikishwaji wa wananchi katika huduma za kifedha, kufuatia kutiwa saini kwa makubaliano ya ushirikiano kati ya Mixx by Yas na Idara ya Maendeleo ya Ushirika Zanzibar.

Akizungumza wakati wa hafla ya utiaji saini wa makubaliano hayo katika maadhimisho ya Siku ya Ushirika Duniani, Mgeni Rasmi, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar anayeshughulikia Sera, Uratibu na Shughuli za Baraza la Wawakilishi, Mhe. Hamza Hassan Juma, alisema ushirikiano huo unaendana na dhamira ya Serikali ya kuharakisha mageuzi ya kidijitali yatakayowezesha vyama vya ushirika kuwa na mifumo ya kisasa, salama na yenye tija.

"Mageuzi ya kidijitali katika sekta ya ushirika yataongeza uwazi, kuimarisha uwajibikaji na kuwapa wananchi huduma bora zaidi za kifedha. Ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi ni muhimu katika kufanikisha maendeleo jumuishi na kujenga uchumi wa kisasa unaomgusa kila Mwananchi," alisema.

Makubaliano hayo yanatarajiwa kunufaisha maelfu ya wanachama wa vyama vya ushirika, vikundi vya kijamii na wajasiriamali Zanzibar kwa kuwezesha usimamizi wa fedha kwa njia za kidijitali, kuongeza usalama wa miamala na kurahisisha upatikanaji wa huduma za kifedha.
Mkurugenzi wa Uzingatiaji wa Sheria wa Mixx Abdallah Nguba alisema ushirikiano huo unaweka msingi wa mageuzi yatakayoboresha namna vyama vya ushirika vinavyosimamia fedha na kutoa huduma kwa wanachama wake kupitia teknolojia.

"Makubaliano haya yanaweka msingi wa mageuzi makubwa katika vyama vya ushirika kwa kuboresha usimamizi wa fedha, kuongeza uwazi na kurahisisha huduma kupitia teknolojia.

Kupitia Mixx Kikoba, wanachama wataweza kuweka akiba, kuchangiana, kufanya malipo, kununua hisa, kupokea gawio na hata kuomba mikopo moja kwa moja kupitia simu zao," alisema.

Aliongeza kuwa vyama vya ushirika vinaendelea kuwa mhimili muhimu wa uchumi kwa kuwaunganisha wakulima, wavuvi, wafugaji na wajasiriamali, huku teknolojia ikichochea uwajibikaji, kumbukumbu sahihi za kifedha na utoaji wa takwimu zitakazosaidia Serikali kupanga maendeleo kwa ufanisi zaidi.

Makubaliano hayo pia yanatarajiwa kuharakisha urasimishaji wa vikundi na vyama vya ushirika, kupunguza matumizi ya fedha taslimu na kuongeza imani ya wanachama kupitia mifumo ya kidijitali iliyo salama na yenye uwazi.

Hatua hiyo inaendelea kuimarisha nafasi ya Mixx kama mshirika wa Serikali katika kukuza ujumuishwaji wa kifedha na kuharakisha uchumi wa kidijitali unaowawezesha wananchi kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya kiuchumi ya Zanzibar na Tanzania kwa ujumla.








Na Mwandishi Wetu
TUME ya Nguvu za Atomiki Tanzania (TAEC) imesema Serikali imeanza maandalizi ya kuanzisha mpango wa kuzalisha umeme wa nyuklia, huku ikisisitiza kuwa utekelezaji wa mradi huo utafuata kikamilifu viwango vya kimataifa vya usalama ili kulinda wananchi, mazingira na kuhakikisha matumizi salama ya teknolojia hiyo.

Akizungumza na waandishi wa habari katika banda la TAEC kwenye Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Mkurugenzi Mkuu wa TAEC, Prof. Najat Kassim Mohammed, amesema Tanzania ipo katika hatua za awali za maandalizi kabla ya kuingia rasmi katika awamu ya kwanza ya utekelezaji wa mpango huo.

Alisema Serikali inaendelea kuimarisha mfumo wa kisheria, sera na taasisi zitakazosimamia matumizi ya teknolojia ya nyuklia ili kuhakikisha uzalishaji wa umeme unafanyika kwa kuzingatia viwango vya usalama vinavyokubalika kimataifa, sambamba na kujenga uelewa wa wananchi kuhusu matumizi ya nishati hiyo.

Prof. Najat alisema TAEC tayari imewaalika wataalamu wa kimataifa kufanya tathmini ya utayari wa Tanzania katika kutekeleza mpango huo.

Alieleza kuwa endapo tathmini hiyo itaridhisha, nchi itapata kibali cha kuendelea na hatua inayofuata ya utekelezaji.

Aidha, alisema Serikali inalenga ndani ya kipindi cha miaka saba kuanza kuzalisha umeme wa nyuklia, hatua inayotarajiwa kuongeza upatikanaji wa nishati ya uhakika, kuimarisha ukuaji wa uchumi na kuchochea maendeleo ya sekta ya viwanda.

Akizungumzia upatikanaji wa malighafi, Prof. Najat amesema Tanzania ina akiba ya madini ya Urani, ambayo ndiyo malighafi muhimu katika uzalishaji wa nishati ya nyuklia kuongeza kuwa madini ya urani lazima yachakatwe kwa teknolojia maalumu kabla ya kutumika kama mafuta ya nyuklia.

Alieleza kuwa katika hatua za mwanzo, urani itakayochimbwa nchini itasafirishwa kwenda nje ya nchi, ikiwemo Urusi, kwa ajili ya kuchakatwa, kisha kurejeshwa Tanzania kwa matumizi ya kuzalisha umeme.

Prof. Najat alisema mradi wa uchimbaji wa madini ya urani unatarajiwa kuanza katika eneo la Mkuju, mkoani Ruvuma, huku shughuli za utafiti zikiendelea katika maeneo mengine ili kubaini akiba zaidi zenye uwezo wa kuchimbwa kibiashara.

Pamoja na hayo, aliwataka wananchi kujenga uelewa sahihi kuhusu teknolojia ya nyuklia na kuondoa hofu zisizo na msingi, akisisitiza kuwa Serikali inatekeleza mpango huo kwa kuzingatia miongozo na viwango vya kimataifa vinavyolenga kuhakikisha usalama wa watu, mazingira na miundombinu.

Alisema matumizi ya teknolojia ya nyuklia yana mchango mkubwa katika maendeleo ya taifa, siyo tu katika uzalishaji wa umeme, bali pia katika sekta za afya, kilimo, viwanda na utafiti wa kisayansi.
Na Mwandishi Wetu
SERIKALI imesema itaendelea kuimarisha programu za ukuzaji wa ujuzi kwa nguvu kazi, kuboresha huduma za umma na kuimarisha mifumo ya ajira, mahusiano kazini pamoja na hifadhi ya jamii ili kujenga uchumi wenye ushindani na kuongeza ustawi wa wananchi.

Hayo yamesemwa na Naibu Waziri katika Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano), Dkt. Evaline Wilbard Munisi, baada ya kutembelea mabanda ya taasisi zilizo chini ya wizara hiyo katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba).

Dkt. Munisi alisema maonesho hayo yamekuwa jukwaa muhimu la kuwafikia wananchi kwa kuwapatia elimu kuhusu sheria za kazi, haki za wafanyakazi, afya na usalama mahali pa kazi pamoja na viwango vya chini vya mishahara, huku taasisi mbalimbali zikiendelea kutoa huduma moja kwa moja kwa wananchi.

Aliwapongeza watumishi wanaohudumu kwenye mabanda hayo kwa weledi, ubunifu na kujituma, akisema juhudi zao zimeongeza uelewa wa wananchi kuhusu masuala ya kazi na kupunguza sintofahamu kupitia elimu ya ana kwa ana.

Aidha, alisema Serikali imeongeza msisitizo katika utekelezaji wa programu za kuwajengea vijana ujuzi unaoendana na mahitaji ya soko la ajira la sasa na la baadaye, ili kuongeza ushindani wa nguvu kazi ya Tanzania.

Alieleza kuwa utekelezaji wa programu hizo unaendelea katika vyuo vya mafunzo ya ufundi na stadi nchini, ambapo Serikali inaendelea kufuatilia maendeleo yake ili kuhakikisha vijana wanapata maarifa na ujuzi unaohitajika katika sekta mbalimbali za uzalishaji.

"Baada ya miaka michache tunaamini Tanzania haitahitaji tena kutegemea wataalamu kutoka nje katika maeneo mengi kwa sababu tunawaandaa wataalamu wetu hapa nchini," alisema Dkt. Munisi.

Aliongeza kuwa hatua hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa maono ya Rais Samia Suluhu Hassan ya kujenga taifa lenye rasilimali watu wenye ujuzi, uwezo wa kushindana na kuchangia maendeleo ya uchumi wa taifa.

Kuhusu mahusiano kazini, Dkt. Munisi alisema Serikali inaendelea kushirikiana na taasisi za dini, vyama vya siasa, mashirika yasiyo ya kiserikali na wadau mbalimbali katika kuimarisha mshikamano wa kitaifa na mahusiano mazuri sehemu za kazi na katika jamii.

"Mahusiano mazuri ndiyo lango la maendeleo," alisema, akitoa wito kwa Watanzania kuendelea kulinda amani, umoja na ushirikiano kwa maslahi ya maendeleo ya nchi.

Katika ziara hiyo, Naibu Waziri alitembelea mabanda ya Taasisi ya Taifa ya Hifadhi ya Jamii (NSSF), Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA) pamoja na Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA), ambapo alijionea namna taasisi hizo zinavyotoa huduma kwa wananchi.

Alizipongeza taasisi hizo kwa kuboresha utoaji wa huduma, akibainisha kuwa matumizi ya mifumo ya kidijitali, hususan katika NSSF, yamerahisisha wanachama kupata taarifa za michango, mafao na huduma nyingine kwa haraka na kwa wakati.

Dkt. Munisi aliwahamasisha wananchi kutembelea mabanda ya Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi nyingine za Serikali katika Maonesho ya Sabasaba ili kujipatia elimu, huduma na taarifa mbalimbali zinazotolewa na taasisi za umma.

Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam yanaendelea kuwa jukwaa muhimu linalowakutanisha taasisi za Serikali, sekta binafsi na washiriki kutoka ndani na nje ya nchi kwa lengo la kuonesha bidhaa, huduma, teknolojia na fursa za biashara na uwekezaji.

Benki ya NMB imesema huduma ya NMB Kikundi Mini App, iliyopo ndani ya NMB Mkononi Super App, imebuniwa kurahisisha usimamizi wa vikundi kwa kuwawezesha wanachama na viongozi kupata huduma za kifedha kidigitali kwa usalama, uwazi na ufanisi zaidi.

Akizungumza katika Banda la NMB kwenye Maonesho ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam, maarufu Sabasaba, Meneja wa Kanda, Huduma za Vikundi na Benki Vijijini wa NMB, Dismas Prosper, alisema mfumo huo unapunguza muda na gharama za kupata huduma za benki, huku ukiimarisha usalama wa miamala na kurahisisha shughuli za vikundi mbalimbali vya kijamii na kiuchumi.

Prosper alisema kupitia NMB Kikundi Mini App, wanachama wa vikundi wanaweza kufungua akaunti bila kutembelea tawi la benki, kufanya miamala kwenda benki nyingine na mitandao ya simu, pamoja na kuweka michango yao moja kwa moja kwenye akaunti ya kikundi. Aidha, alisema kila mwanachama hupokea ujumbe mfupi wa simu unaothibitisha mchango uliowekwa, hatua inayoongeza uwazi na uwajibikaji katika usimamizi wa fedha za kikundi.

Aliongeza kuwa mfumo huo pia unawawezesha wanachama kuona taarifa za hisa, idadi na majina ya wanachama wa kikundi, pamoja na taarifa binafsi za kila mwanachama kulingana na mamlaka aliyopewa ndani ya mfumo. Prosper alisema ubunifu huo ni sehemu ya jitihada za NMB kuendelea kuleta suluhisho za kidigitali zinazowawezesha wananchi, hususan vikundi vya kijamii na kiuchumi, kupata huduma za kifedha kwa urahisi, usalama na uwazi zaidi.









Na Oscar Assenga,TANGA


Wazazi, walezi na waajiri nchini wamehimizwa kuhakikisha watoto wanawakatia bima ya afya mapema ili kuwaepusha na changamoto za gharama kubwa za matibabu na kuwawezesha kupata huduma za afya kwa wakati wanapougua.

Wito huo umetolewa leo na Afisa Matekelezo wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) Mkoa wa Tanga, Macrina Clemens, wakati wa utoaji wa elimu kuhusu bima ya afya ulioambatana na zoezi la upimaji wa afya na usajili wa wanachama wa vifurushi mbalimbali katika Kanisa la KKKT Ushirika wa Makorora, jijini Tanga.



Akizungumza na waumini wa kanisa hilo, Macrina alisema afya ni mtaji muhimu kwa maendeleo ya familia na Taifa, hivyo kujiunga na bima ya afya ni uwekezaji unaowalinda wananchi dhidi ya gharama zisizotarajiwa za matibabu.

Alisema wazazi wanaowakatia watoto wao bima ya afya hupata uhakika wa matibabu wakati wowote mtoto anapougua, jambo linalowapa utulivu wa akili na kuwawezesha watoto kuendelea na masomo bila kukatishwa na changamoto za kifedha.



“Mzazi anapokuwa na bima ya afya kwa mtoto wake anakuwa na uhakika wa kupata matibabu kwa wakati, hivyo kuepuka usumbufu wa kutafuta fedha za dharura kila ugonjwa unapojitokeza,” alisema.

Macrina alisema wanafunzi wanaosoma katika shule mbalimbali wanaweza kujiunga na bima ya afya kupitia shule zao kwa gharama ya Sh50,400 kwa mwaka mzima wa masomo, huku watoto ambao bado hawajaanza shule wakijiunga kupitia vifurushi mbalimbali vinavyotolewa na NHIF.



Alisema Serikali inaendelea kutekeleza azma ya kuhakikisha kila Mtanzania anakuwa na bima ya afya, hivyo akazitaka taasisi za elimu, wazazi, walezi, waajiri na wamiliki wa kampuni binafsi kutumia fursa hiyo kuwaandikisha watoto na wafanyakazi wao.

“Bima ya afya si gharama, ni kinga ya maisha. Ukiwa na bima unakuwa na uhakika wa kupata daktari, dawa na huduma za matibabu bila kubeba mzigo mkubwa wa kifedha pale unapougua,” alisema.



NHIF imeendelea kutoa elimu kwa makundi mbalimbali ya wananchi kuhusu umuhimu wa bima ya afya ikiwa ni sehemu ya juhudi za Serikali za kuongeza idadi ya Watanzania wanaonufaika na huduma hiyo na kuimarisha upatikanaji wa huduma bora za afya nchini.




Na John Mapepele, Shanghai-China

Waziri wa Afya wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mohamed Mchengerwa ametoa mwito wa mashirikiano ya kisayansi katika utafiti ugonjwa wa kifua kikuu baina ya Tanzania na China ili kuutibu ugonjwa huo katika kipindi kifupi tofauti na hali ilivyo sasa.

Mchengerwa ametoa mwito huo leo katika Kituo cha Shanghai Sci-Tech Inno Center for Infection & Immunity kilichopo Shanghai, nchini China akipendekeza ushirikiano wa kimkakati kati ya Tanzania na China unaolenga utafiti wa kifua kikuu (TB), ubunifu wa kitabibu, na maendeleo ya dawa.

Katika hotuba yake, mbele ya wanasayansi wabobezi wa utafiti akiwemo Mkurugenzi Dkt. Zhang Wenhong, pamoja na wawakilishi wa Chuo Kikuu cha Fudan na Hospitali Maarufu ya Huashan ya nchinib China, amesisitiza umuhimu wa ushirikiano wa kimataifa katika sayansi ya magonjwa ya kuambukiza.

Waziri Mchengerwa ambaye ameongoza Timu ya wataalam kutoka Tanzania na Naibu Katibu Mkuu anayeshughulikia Dawa na vifaaa tiba Emmanuel Tayari ametembelea maabara ya kituo hicho na kijionea vifaa vya kisasa vya uchunguzi wa magonjwa mbalimbali.

Waziri amekipongeza Kituo cha Shanghai Sci-Tech Inno Center for Infection & Immunity kuwa miongoni mwa vitovu kinachoongoza duniani ambapo utafiti wa kisasa kuhusu maambukizi, kinga ya mwili, na usalama wa kibaiolojia unatafsiriwa kuwa matokeo halisi ya kitabibu.

Amependekeza kuanzisha ushirikiano rasmi kati ya kituo hicho cha Shanghai na Hospitali ya Kibong'oto ambayo ameielezea kuwa ni taasisi ya kihistoria inayojihusisha na matibabu na utafiti wa kifua kikuu nchini Tanzania kwa mafanikio makubwa.

Aidha, Waziri Mchengerwa amesisitiza kuwa kila taasisi ina nguvu zake za kipekee: Shanghai ina uwezo mkubwa katika genomiki, kinga ya mwili (immunology), uchunguzi wa magonjwa, na sayansi ya kompyuta, wakati Kibong'oto inatoa uzoefu wa karibu karne moja wa kliniki katika udhibiti wa TB, ikiwa ni pamoja na nyaraka adimu za kihistoria za wagonjwa zinazoanzia mwaka 1926.

"Hospitali ya Kibong'oto liyopo katika miteremko ya Mlima Kilimanjaro katika Mkoa wa Kilimanjaro ilianzishwa mwaka 1926 kama sanatorium ya kifua kikuu. Baada ya muda, ilibadilika kutoka kituo cha matibabu hadi hospitali ya rufaa ya kitaifa ya kisasa, na tangu 2006 imekuwa kituo cha kitaifa cha Tanzania cha kifua kikuu sugu". Amefafanua Mhe. Mchengerwa

Amependekeza hospitali ya Kibong'oto kuweka nyaraka zake yenye zaidi ya miaka 100 katika mfumo wa kidijitali na kuzichambua kisayansi ili kufungua njia mpya za kuelewa usugu wa dawa na mabadiliko ya magonjwa, hasa zikichanganywa na zana za kisasa za matibabu ya ugonjwa huo zinazopatikana katika Kituo cha Shanghai.

Ameyataja baadhi ya maeneo muhimu ya ushirikiano kuwa ni pamoja na Utafiti wa TB sugu ya dawa, unaolenga epidemiolojia ya molekuli na uchunguzi wa haraka unaofaa mazingira halisi ya kliniki.

Mabadilishano ya kitaaluma na kitabibu, kuruhusu wataalamu wa Tanzania na China kujifunza katika taasisi za kila upande

Uwekaji kidijitali wa nyaraka za kihistoria za Kibong'oto, kubadilisha data ya miongo mingi kuwa rasilimali ya kisasa ya utafiti na

Kuimarisha mifumo ya maabara na ufuatiliaji nchini Tanzania, kusaidia ufuatiliaji wa ugonjwa huo.Pia Waziri Mchengerwa ameeleza kuwa dhamira ya Serikali ya Tanzania ni kuhama kutoka kuagiza dawa hadi kuzalisha ndani ya nchi.

Alialika ushirikiano na washirika wa China kusaidia uzalishaji wa ndani wa dawa za TB, vifaa vya uchunguzi, na huenda hata chanjo za baadaye ambapo ingejumuisha uhamishaji wa teknolojia, mafunzo ya wataalamu, na ujenzi wa mifumo ya ubora wa uzalishaji ndani ya Tanzania.

" Hili si tu lengo la kiuchumi, bali ni suala la uhuru wa kisayansi na ustahimilivu wa muda mrefu wa afya ya umma". Amesisitiza Mchengerwa

Pia amesisitiza kuwa miundombinu itakayojengwa kupitia ushirikiano huu inaweza kuwa msingi wa kukabiliana na magonjwa mapya ya milipuko katika siku zijazo ambapo amesema mchanganyiko wa uzoefu wa kliniki wa Tanzania na uwezo wa utafiti wa China utaimarisha maandalizi ya kimataifa dhidi ya magonjwa yanayoibuka.

Akihitimisha hotuba, Waziri alisisitiza tena dhamira ya Tanzania ya kushirikiana badala ya kutegemea misaada, akisisitiza uwekezaji katika taasisi za kitaifa na uwezo wa kisayansi.

Alitoa mwito wa moja kwa moja kwa Mkurugenzi Zhang na wenzake Shanghai kuhamia kutoka majadiliano kwenda makubaliano rasmi na utekelezaji—akiona ushirikiano huo kama daraja la muda mrefu kati ya uzoefu wa kitabibu Afrika Mashariki na ubunifu wa kibayomedisini China.

"Iwapo utatekelezwa, mpango huu unaweza kuwa mfano adimu wa ushirikiano wa usawa katika afya ya kimataifa—ukiunganisha uzoefu wa muda mrefu wa kliniki na sayansi ya kisasa katika juhudi ya pamoja ya hatimaye kuishinda kifua kikuu". Amefafanua Mchengerwa.






Na Mwandishi Wetu 

BODI ya Utalii Tanzania (TTB) imemkabidhi rasmi mwanautalii na mtangazaji wa vivutio vya utalii kutoka Oman, Khalid Hamed Al Barwani, Ubalozi wa Hiari wa Utalii wa Tanzania, ikiwa ni hatua ya kimkakati ya kuimarisha juhudi za kuitangaza Tanzania katika masoko ya kimataifa na kuongeza idadi ya watalii wanaotembelea nchini.

Ubalozi huo umekabidhiwa na Mkurugenzi Mkuu wa TTB, Ephraim Mafuru, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, ikiwa ni kutambua mchango mkubwa wa Al Barwani katika kuitangaza Tanzania kupitia majukwaa mbalimbali ya kimataifa.

Al Barwani alipata umaarufu mkubwa baada ya kuongoza kundi la Dream Team Explorers kutembelea Shamba la Miti la Sao Hill mwaka 2024, ambapo walijionea vivutio vya kipekee vinavyopatikana katika eneo hilo, ikiwemo misitu ya kupandwa, mandhari ya kuvutia ya asili na eneo la Mto Ruaha. 

Maudhui waliyoyashiriki kupitia majukwaa yao ya kidijitali yalichangia kuongeza mwonekano wa Sao Hill na kuibua hamasa ya watalii wa ndani na nje ya nchi kutembelea eneo hilo.

Akizungumza wakati wa hafla ya kukabidhi ubalozi huo, Mafuru alisema TTB itaendelea kushirikiana na watu mashuhuri, watengeneza maudhui na wadau wa kimataifa wenye ushawishi mkubwa katika masoko mbalimbali ili kuendelea kuitangaza Tanzania kama moja ya vivutio bora vya utalii duniani.

“Ubalozi huu ni kutambua mchango wa Khalid Al Barwani katika kuitangaza Tanzania na ni sehemu ya mkakati wetu wa kupanua wigo wa masoko ya utalii kupitia mabalozi wa hiari wanaotumia ushawishi wao kufikisha ujumbe wa Tanzania kwa mamilioni ya watu duniani,” alisema Mafuru.

Kwa upande wake, Al Barwani alishukuru kwa heshima hiyo na kuahidi kuendelea kuitangaza Tanzania kupitia majukwaa yake ya kimataifa, akieleza kuwa nchi ina vivutio vya kipekee vinavyostahili kufahamika zaidi duniani.

“Tanzania ni nchi yenye uzuri wa kipekee, kuanzia hifadhi za wanyamapori, misitu, fukwe, utamaduni hadi ukarimu wa wananchi wake. Nitaendelea kuwa balozi wa kuitangaza Tanzania kwa dunia,” alisema.

TTB inaendelea kutumia ushirikiano na wadau wa kimataifa pamoja na mabalozi wa hiari wa utalii kama sehemu ya mkakati wa kuongeza ushindani wa Tanzania katika soko la utalii duniani na kuunga mkono malengo ya taifa ya kukuza sekta ya utalii, kuongeza idadi ya wageni wa kimataifa na kuongeza mchango wa sekta hiyo katika maendeleo ya uchumi wa nchi.







Kulikuwa na wakati ambapo michezo ya kasino mtandaoni ilihitaji kitu zaidi ya picha nzuri na mizunguko ya kawaida ili kuwafanya watu wavutiwe. Katika dunia ya burudani ya kidijitali ambayo kila sekunde inaleta jambo jipya, Meridianbet imeleta mchezo ambao unafungua ukurasa mpya wa msisimko na furaha kupitia Wild 4th Fruits kutoka Expanse. Mchezo huu mpya umeingia sokoni ukiwa na mwonekano wa kuvutia, rangi ang’avu, na mfumo wa uchezaji unaokufanya ujisikie kama umeingia katika ulimwengu wa matunda wenye nguvu, nishati na zawadi za kusisimua.

Wild 4th Fruits si sloti ya mchezo mchezo. Mara tu unapofungua mchezo huu, unakaribishwa na mazingira yenye rangi za kuvutia ambazo zinawakilisha nguvu na uhai wa matunda mbalimbali. Kila ukicheza, matarajio ya ushindi na burudani huungana katika namna ya kipekee. Expanse wamefanikiwa kuunda mchezo ambao unawapa wachezaji uzoefu wa kisasa ambao wengi wameupenda kwa miaka mingi.

Meridianbet haikuachi nyuma, kuna michezo mbalimbali ya kasino mtandaoni pamoja na mechi za kimataifa za kubashiri zenye odds bomba na nafasi ya kuongeza kipato chako kila siku. Kujiunga ni rahisi! Tembelea tovuti ya MERIDIANBET au piga *149*10#.

Kwa wabashiri wanaopenda michezo yenye uchezaji mwepesi lakini yenye uwezo wa kukuweka kwenye hali ya kusisimka kwa muda mrefu, basi Wild 4th Fruits imekuja na kile ambacho wengi wamekuwa wakikitafuta. Mfumo wake wa uchezaji ni rahisi kuelewa, jambo linalomfanya kila mchezaji, iwe ni mzoefu au anayeanza, aweze kufurahia mchezo bila changamoto yoyote.

Katika kipindi hiki ambapo vijana wengi wanatafuta njia mpya za kujiburudisha kupitia simu zao na vifaa vya kidijitali, Meridianbet imeendelea kuonyesha kwa nini ni moja ya majukwaa yanayoongoza kwa kuleta michezo ya kisasa yenye ubunifu. Wild 4th Fruits ni ushahidi mwingine kwamba burudani ya mtandaoni inaweza kuwa rahisi, yenye kuvutia, na yenye uwezo wa kutoa ushindi ambao unakufanya utake kurejea tena na tena.

Ikiwa wewe ni mmoja wa wale wanaopenda kujaribu vitu vipya, kufurahia ushindi na msisimko wa kila mchezo, basi Wild 4th Fruits inastahili kuwa kwenye orodha yako ya kwanza ya kujaribu ndani ya Meridianbet. Huu mchezo ni safari kamili ya burudani ambayo imebeba furaha, ushindi, na uwezekano wa kufanya kila dakika yako kuwa ya kipekee.

Mechi ya leo kati ya Mexico na England ni pambano la kihistoria katika hatua ya 16 Bora, inayochezwa kwenye Uwanja wa Estadio Azteca. Ingawa historia inaonyesha ubabe wa England, ambapo wameshinda mara 6 kati ya 9 dhidi ya Mexico, mechi hii ina mazingira tofauti kabisa. England anajua kwamba Mexico katika uwanja wao wa nyumbani, hasa Azteca, ni timu tofauti, na kila kitu kinaweza kutokea.

Mexico wana rekodi ya kustaajabisha kwenye Uwanja wa Azteca; katika mechi 89 za mashindano, wameshinda 70, sare 17, na kushingwa mara 2 tu, toka mwaka 2013. Uwepo wa mashabiki na mwinuko wa zaidi ya mita 2000 ni silaha kubwa kwa wenyeji. England wana kumbukumbu mbaya humu, wakitolewa na Argentina mwaka 1986 baada ya bao la "Mkono wa Mungu" la Diego Maradona.

Mexico wamekuwa na mwendo mzuri, wakishinda mechi zote nne na wastani wa mabao 8-0, huku Raul Jimenez akiongoza safu ya ushambuliaji. Kocha Javier Aguirre anatumia mbinu za kukaba mapema na kupiga mpira wa kasi, hasa kupitia Gilberto Mora, ili kuwachosha wapinzani kwenye mwinuko. England walikaribia kuondolewa na DR Congo, wakiokolewa na mabao mawili ya Harry Kane, na kocha Thomas Tuchel anajua kwamba wanapaswa kuboresha sana ili kushinda.

Ingia kwenye kasi ya kujishindia pesa kwenye michezo ya Kasino ya Mtandaoni kama vile, Keno, Aviator, Poker, Roulette, Wild Icy Fruits, Super Heli na mingine kibao. Jiunge leo kwa kutembelea tovuti ya meridianbet.co.tz au piga *149*10# kisha uanze safari yako ya ushindi.

Mexico wanatarajia kutumia fursa ya uwanja wa nyumbani na mbinu zao za kukaba mapema kuzuia mchezo wa England. Walakini, England wana ubora wa kimataifa kama Harry Kane na Jude Bellingham, ambao wanaweza kuamua mechi kwa kipaji chao. England wanahitaji kuvumilia shinikizo na kuzuia makosa ya nyuma, hasa dhidi ya wapinzani kama Julian Quinones.

Pambano hili ni la kusisimua, likiwa na Mexico wanaotaka kuvunja rekodi yao ya kutofika robo fainali tangu 1986, na England wanaotaka kuendeleza ndoto yao ya michuano ya dunia. Ingawa England wana historia nzuri, Mexico wana silaha za kutosha kusababisha mshtuko, na ushindi wowote utakuwa wa maana kwa nchi husika.

-Wasema unaongeza uwazi, ufanisi na kuokoa muda wa kupata huduma


Na Grace Michael, Dar es Salaam

WANANCHI na wanachama wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) wamepongeza Mfumo wa Kujihudumia Binafsi (Self Service) unaowezesha wanachama kupata huduma mbalimbali kupitia simu janja, wakisema mfumo huo umeongeza uwazi katika utoaji wa huduma, kurahisisha upatikanaji wa taarifa na kuokoa muda ambao awali walilazimika kuutumia kufika katika ofisi za NHIF.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti walipotembelea banda la NHIF katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, wananchi hao walisema maboresho ya mifumo ya kidijitali ya NHIF yameongeza ufanisi na kuimarisha usimamizi wa huduma za bima ya afya.

Bw. Emmanuel Selemani alisema mfumo huo unampa mwanachama uwezo wa kuona historia ya huduma zote alizopata katika vituo vya kutolea huduma za afya, hatua inayochangia kuongeza uwazi na kuwapa wanachama nafasi ya kushiriki katika kulinda rasilimali za Mfuko.

"Mfumo huu ni mzuri sana kwa sababu kila mwanachama anaweza kuona huduma alizopata katika kituo cha afya. Ikitokea kuna huduma zimeonekana kwenye mfumo lakini hakuzipata, anaweza kutoa taarifa NHIF ili zifuatiliwe. Hii itasaidia kudhibiti na kuzuia vitendo vya udanganyifu katika utoaji wa huduma," alisema.

Kwa upande wake, Bi. Maria Nzalima alisema ameridhishwa na huduma zinazotolewa katika banda la NHIF kwenye maonesho hayo kutokana na kasi ya utoaji wa huduma pamoja na elimu aliyopata kuhusu haki na wajibu wa mwanachama wa NHIF.

"Huduma ni za haraka na nimepata elimu muhimu kuhusu namna ya kutumia bima yangu pamoja na haki na wajibu wangu kama mwanachama. Hii imeniongezea uelewa na kujiamini ninapotumia huduma za NHIF," alisema.

Akizungumza kuhusu huduma zinazotolewa katika banda la NHIF, Ofisa Uanachama Mwandamizi, Bw. Hassan Ally, alisema wananchi wanapata huduma mbalimbali ikiwemo usajili kupitia vifurushi mbalimbali vya bima ya afya, elimu ya matumizi ya Mfumo wa Self Service, uhuishaji wa taarifa za wanachama, kubadilisha namba za simu pamoja na kuunganisha taarifa zao na Mfumo wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA).

Aliongeza kuwa maonesho hayo yanatoa fursa muhimu kwa wananchi kupata elimu kuhusu huduma za NHIF na kujisajili ili waweze kunufaika na huduma za bima ya afya.

"Tunawahamasisha wananchi wote kutembelea banda la NHIF lililopo ndani ya Banda la Kijiji cha Bima ili kupata elimu, kujisajili na kufahamu huduma mbalimbali zinazotolewa na Mfuko kwa wanachama wake," alisema.

NHIF imeendelea kushiriki Maonesho ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam kila mwaka ikiwa ni sehemu ya jitihada za kusogeza huduma kwa wananchi, kutoa elimu kuhusu bima ya afya na kuhamasisha ushiriki katika utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote. ”Bima ya Afya kwa Wote, Jiunge Sasa."







Top News