Na Janeth Raphael - MichuziTv 

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, amewataka wananchi wanaomiliki silaha kuhakikisha wanakamilisha taratibu zote za kisheria na vibali vinavyohitajika kabla ya Agosti 30, 2026, akieleza kuwa operesheni maalum ya ukaguzi wa silaha itaanza mara baada ya muda huo.

Chalamila ametoa agizo hilo wakati akizungumza na waandishi wa habari leo , akisisitiza kuwa wamiliki ambao kwa sababu mbalimbali, ikiwemo kusahau au kutokuwa na uelewa wa kutosha kuhusu taratibu, hawajakamilisha malipo ya vibali au hatua nyingine za kisheria, wanapaswa kutumia muda uliopo kufika katika mamlaka husika na kurekebisha hali hiyo.

Amesema hatua hiyo inalenga kuhakikisha silaha zinazomilikiwa na wananchi katika Mkoa wa Dar es Salaam zinakuwa na kumbukumbu na vibali halali vinavyotambulika kisheria, kabla ya kuanza kwa operesheni hiyo.

Kwa upande mwingine, Mkuu huyo wa Mkoa amewataka watu wanaomiliki silaha bila kufuata sheria kuzisalimisha kwa hiari katika Jeshi la Polisi au kituo cha Polisi kilicho karibu kabla ya operesheni kuanza. Amesisitiza kuwa hatua hiyo inaweza kusaidia wahusika kuepuka kukumbana na hatua za kisheria zitakazochukuliwa baada ya ukaguzi kuanza.

Aidha, Chalamila ametoa mwito kwa familia ambazo ndugu zao wamefariki huku wakiacha silaha zenye vibali halali kuhakikisha hazizifichi wala kuzihamisha bila kufuata utaratibu. Badala yake, amewataka kuwasilisha taarifa pamoja na silaha hizo kwa mamlaka husika ili kupata maelekezo ya kisheria kuhusu namna ya kushughulikia umiliki huo.

Kuhusu silaha zinazoripotiwa kuibiwa, amewataka wamiliki kutoa taarifa Polisi na kufuata taratibu zote zinazohitajika. Amesisitiza kuwa silaha hizo zinapopatikana, wahusika hawapaswi kuzificha au kuendelea kuzitumia bila kufuata maelekezo ya mamlaka.

Chalamila amesisitiza kuwa Agosti 30, 2026 ndiyo mwisho wa muda uliotolewa kwa wamiliki kuhakikisha wanakamilisha taratibu zao, akieleza kuwa baada ya tarehe hiyo operesheni maalum ya ukaguzi itaanza na yeyote atakayebainika kumiliki silaha kinyume cha sheria atachukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria.

Amewataka wananchi kutotumia muda uliobaki kupuuza agizo hilo, bali kuhakikisha mapema kuwa umiliki wa silaha zao uko katika hali halali na unaotambulika na mamlaka, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha udhibiti na usalama wa silaha katika Mkoa wa Dar es Salaam.






Na Mwandishi Wetu
WATANZANIA wameanza kunufaika na huduma za matibabu ya kibingwa zinazopatikana nchini, hali inayopunguza gharama na ulazima wa kusafiri nje ya nchi kutafuta matibabu.

Mkurugenzi Mtendaji wa Universal Medical Tourism, Dkt. Sharif Mollel, amesema huduma hizo zinapatikana katika Hospitali ya SINO iliyopo Mikocheni, Dar es Salaam.

Amesema kampuni yake inashirikiana na hospitali hiyo kurahisisha upatikanaji wa huduma za kibingwa, teknolojia za kisasa za matibabu pamoja na baadhi ya huduma za tiba za jadi za China, zinazojulikana kama Traditional Chinese Medicine. Amesema uwepo wa huduma hizo nchini unawapa Watanzania nafasi ya kupata matibabu bila kuingia gharama za tiketi za ndege, malazi, visa na matumizi mengine yanayotokana na safari za matibabu nje ya nchi.

“Lengo letu ni kuona Watanzania wanapata huduma nyingi zaidi hapa nchini. Kama huduma inayohitajika inapatikana Tanzania, hakuna sababu ya mgonjwa kuanza na safari ya kwenda nje ya nchi,” amesema.

Amesema baadhi ya wagonjwa kutoka nchi za Afrika Mashariki na ukanda wa SADC pia wameanza kuja Tanzania kupata huduma katika hospitali hiyo. Kwa mujibu wa Dkt. Mollel, hatua hiyo inaonesha kuwa Tanzania ina nafasi ya kujijenga kuwa kituo muhimu cha huduma za afya na medical tourism katika ukanda wa Afrika.

“Tunataka kuona medical tourism ikienda pande zote. Siyo Watanzania kwenda nje kutibiwa pekee, bali pia wagonjwa kutoka nchi nyingine kuja Tanzania kupata huduma,” amesema.

Amesema Hospitali ya SINO inatoa huduma mbalimbali za uchunguzi na matibabu kwa kutumia teknolojia za kisasa, zikiwemo huduma za mifupa na viungo, mgongo, mfumo wa neva, urology na physiotherapy. Hospitali hiyo pia ina teknolojia za uchunguzi zikiwemo Ultrasound, CT Scan na MRI, zinazosaidia madaktari kufanya uchunguzi wa kina kabla ya kuamua aina ya matibabu anayohitaji mgonjwa.

Mbali na tiba za kisasa, amesema Hospitali ya SINO inatoa baadhi ya huduma za Traditional Chinese Medicine, ikiwemo acupuncture, inayotumia sindano maalumu katika maeneo mahususi ya mwili chini ya usimamizi wa wataalamu. Amesema huduma hizo zinaweza kusaidia katika usimamizi wa baadhi ya hali za maumivu, misuli na viungo baada ya mgonjwa kufanyiwa tathmini ya kitaalamu.

Dkt. Mollel amesisitiza kuwa huduma za tiba za jadi za China hazikusudii kuchukua nafasi ya tiba za kisasa, bali hutolewa kulingana na ushauri na tathmini ya wataalamu. Ametoa wito kwa Watanzania, hususan wakazi wa Dar es Salaam, kutumia nafasi ya kuwepo kwa huduma hizo nchini kabla ya kufanya uamuzi wa kusafiri nje ya nchi kutafuta matibabu.

Dkt. Mollel amesema moja ya malengo ya Universal Medical Tourism ni kuendelea kuvutia wataalamu, teknolojia na uwekezaji wa afya kutoka nje ya nchi ili huduma nyingi zaidi zipatikane Tanzania. Amesema kampuni hiyo pia inalenga kuendeleza ushirikiano kati ya madaktari wa Tanzania na wataalamu kutoka China kupitia kambi za matibabu na programu mbalimbali za kubadilishana ujuzi.

“Tunapotengeneza mazingira ya daktari wa Tanzania kufanya kazi pamoja na mtaalamu kutoka China, tunamhudumia mgonjwa lakini pia tunajenga uwezo wa wataalamu wetu,” amesema. Amesema hatua hiyo inaweza kusaidia teknolojia na maarifa yanayoletwa nchini kubaki na kutumika kwa muda mrefu badala ya huduma kutegemea wataalamu wa nje pekee.

Dkt. Mollel amesema dhamira ya muda mrefu ni kuona Tanzania inapunguza idadi ya wagonjwa wanaolazimika kusafiri nje kwa huduma zinazoweza kutolewa nchini, huku ikiongeza idadi ya wagonjwa kutoka mataifa mengine wanaokuja kupata matibabu hapa nchini.

 

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amewasili Zanzibar, leo tarehe 11 Agosti 2026. Makamu wa Rais anatarajiwa kuwa Mgeni Rasmi katika Ufunguzi wa Jengo la Dakhalia katika Skuli ya Sekondari ya Hasnuu Makame – Kibuteni Unguja, ikiwa ni shamrashamra ya Tamasha la Kizimkazi. (Kizimkazi Festival 2026)



Dodoma, 8 Agosti 2026
RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema Serikali itaendelea kutafuta na kufungua masoko ya ndani na nje ya nchi kwa ajili ya mazao ya kilimo, mifugo na uvuvi, hatua inayolenga kuwawezesha wazalishaji kupata masoko ya uhakika na kuongeza tija katika sekta za uzalishaji.

Rais Samia ameyasema hayo leo, Agosti 8, 2026, wakati akizungumza katika maadhimisho ya Siku ya Wakulima (Nane Nane) Kitaifa yaliyofanyika katika Viwanja vya John Malecela, Nzuguni, Dodoma. Amesema Tanzania imeendelea kufungua milango zaidi kwa biashara na uwekezaji, huku Serikali ikiweka mazingira wezeshi kwa wazalishaji na wawekezaji wa ndani na nje ya nchi.

Katika kuimarisha uzalishaji wa ndani, Kiwanda cha K4 cha Kilombero Sugar kimetajwa kuwa uwekezaji muhimu katika kuongeza uzalishaji wa sukari nchini, kupunguza utegemezi wa bidhaa hiyo kutoka nje ya nchi na kuchangia katika safari ya Tanzania kuelekea kujitosheleza kwa sukari.

Akizungumza na waandishi wa habari katika Maonesho ya Nane Nane, Meneja wa Mawasiliano na Mahusiano na Wadau wa Kilombero Sugar, Bw. Victor Byemelwa, amesema kampuni inajivunia uwekezaji wa K4 ambao umeongeza uwezo wa uzalishaji wa sukari na unatarajiwa kuchochea ukuaji wa kilimo cha miwa pamoja na uchumi wa maeneo yanayozunguka shughuli za kampuni.

Amesema uwekezaji huo hauishii katika uzalishaji wa sukari pekee, bali pia una uwezo wa kuongeza uzalishaji wa umeme kutokana na matumizi ya mabaki ya miwa, hatua inayoweza kuchangia katika kuimarisha upatikanaji wa nishati na kuongeza mchango wa kampuni katika gridi ya Taifa.

"Uwekezaji wa K4 ni hatua kubwa katika kuongeza uzalishaji wa sukari nchini. Pamoja na kuongeza uzalishaji, unafungua fursa nyingi zaidi kwa wakulima wa miwa, ajira, biashara na shughuli nyingine ndani ya mnyororo wa thamani wa kilimo," amesema Byemelwa.

Ametoa wito kwa wananchi, hususan wakulima, kutumia fursa zinazotokana na uwekezaji huo kwa kushiriki kikamilifu katika kilimo cha miwa na shughuli mbalimbali zinazohusiana na mnyororo wa thamani, akisema ukuaji wa sekta ya sukari una uwezo wa kuongeza kipato cha kaya na kuchochea maendeleo ya kiuchumi katika jamii.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Masuala ya Ushirikiano na Mawasiliano wa Kilombero Sugar, Bw. Derick Stanley, amesema kampuni imejipanga kuongeza uzalishaji wa sukari nchini ili kukidhi mahitaji ya soko la ndani na kuchangia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Stanley amesema katika kuongeza uzalishaji wa miwa, Kilombero Sugar inatarajia kushirikiana na wakulima wa nje ya mashamba ya kampuni ambao wanakadiriwa kuzalisha takribani tani milioni 1.5 za miwa, hatua inayotarajiwa kuwawezesha wakulima hao kupata zaidi ya shilingi bilioni 150, hivyo kuongeza kipato cha kaya na kuchochea shughuli za kiuchumi katika maeneo ya uzalishaji.

"Tunaendelea kuangalia fursa za kuongeza uzalishaji na kujenga uwezo wa muda mrefu wa sekta ya sukari. Uwekezaji huu unalenga si tu kuongeza uzalishaji wa sukari, bali pia kuimarisha mnyororo wa thamani, kuongeza fursa kwa wakulima na kuchangia katika maendeleo ya viwanda nchini," amesema Stanley.

Akizungumzia ushiriki wa Kilombero Sugar katika Maonesho ya Nane Nane jijini Dodoma, Mkurugenzi wa Biashara wa Kilombero Sugar, Bw. Fimbo Butala, amesema pia kampuni imetumia maonesho hayo kusogeza bidhaa na huduma zake karibu na wananchi, huku ikitoa elimu kuhusu uzalishaji wa sukari, kilimo cha miwa na mchango wa kampuni katika maendeleo ya sekta ya kilimo na viwanda.

Amesema Nane Nane ni jukwaa muhimu la kukutana moja kwa moja na wakulima, wateja na wadau wengine wa sekta ya kilimo, kusikiliza maoni yao na kujenga ushirikiano unaolenga kukuza uzalishaji na kuongeza thamani katika mnyororo wa kilimo.

Na Janeth Raphael - MichuziTv

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, amewapa muda wa wiki moja wamiliki na waendeshaji wa kampuni za mabasi makubwa ya mikoani kuhakikisha wanaanza kutumia Stendi ya Magufuli kama kituo cha kuanzia na kumalizia safari zao, katika hatua inayolenga kupunguza msongamano wa magari katikati ya Jiji la Dar es Salaam.

Chalamila ametoa agizo hilo leo jijini Dar es katika Mkutano na waandishi wa habari ambapo amesema mabasi hayo hayatapaswa tena kuingia katikati ya jiji kwa ajili ya kupakia na kushusha abiria, isipokuwa kampuni sita ambazo tayari zimepewa vibali maalum vya kushusha abiria katika maeneo ya katikati ya jiji. 

Kwa mujibu wa Mkuu huyo wa Mkoa, kampuni nyingine zote zinatakiwa kutumia Stendi ya Magufuli na kuzingatia utaratibu mpya uliowekwa na Serikali.

Chalamila amesema wamiliki na waendeshaji wa mabasi hayo wametakiwa kutumia muda uliopo hadi Agosti 17, 2026 kufanya maandalizi muhimu, huku utekelezaji wa agizo hilo ukianza rasmi baada ya tarehe hiyo. 

Amesema hatua hiyo ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kuboresha mfumo wa usafiri na kupunguza msongamano unaoendelea kujitokeza katika maeneo mbalimbali ya katikati ya Jiji la Dar es Salaam.

Ameeleza kuwa mabasi makubwa yanapoingia katikati ya jiji kwa ajili ya kushusha au kupakia abiria, yanaongeza idadi ya magari katika maeneo ambayo tayari yana msongamano mkubwa, hivyo matumizi ya Stendi ya Magufuli yatasaidia kuyapunguza mabasi hayo katika maeneo ya katikati ya jiji na kuweka utaratibu mzuri wa usafirishaji wa abiria wanaoingia au kutoka Dar es Salaam.

Chalamila amesema abiria watakaofikishwa katika Stendi ya Magufuli hawataachwa bila usafiri wa kuendelea na safari zao, kwani wataweza kutumia huduma mbalimbali za usafiri wa ndani kuelekea maeneo wanayokwenda. 

Miongoni mwa usafiri huo ni mabasi ya mwendokasi, daladala, bajaji na pikipiki, huku kampuni za mabasi zikiruhusiwa pia kuweka huduma za shuttle kwa ajili ya kuwasaidia abiria kutoka stendi hiyo kwenda maeneo mbalimbali ya jiji.

Kwa mujibu wa Chalamila, utaratibu huo hautalenga tu kupunguza msongamano wa magari, bali pia unalenga kulinda na kuongeza fursa za ajira na biashara kwa waendeshaji wa usafiri wa ndani. 

Amesema mabasi makubwa yanapoingia hadi katikati ya jiji na kufanya shughuli ambazo zinaweza kufanywa na watoa huduma za usafiri wa ndani, yanaathiri moja kwa moja shughuli za kiuchumi za kundi hilo la wadau.

Amesema mfumo huo mpya utawezesha kuwepo kwa mgawanyo mzuri wa majukumu katika sekta ya usafirishaji, ambapo mabasi makubwa yatabeba abiria kutoka mikoa mbalimbali na kuwafikisha katika Stendi ya Magufuli, kisha usafiri wa ndani kuchukua jukumu la kuwaunganisha abiria hao na maeneo mbalimbali ndani ya Dar es Salaam.

Chalamila amewataka wamiliki na waendeshaji wa mabasi makubwa kutumia muda uliotolewa kufanya maandalizi ya kutosha, ikiwemo kupanga namna ya kuwasaidia abiria wao kuendelea na safari kutoka Stendi ya Magufuli. 

Amesisitiza kuwa baada ya Agosti 17, 2026, utekelezaji wa utaratibu huo utaanza rasmi, huku kampuni ambazo hazina vibali maalum vya kushusha abiria katikati ya jiji zikitarajiwa kuzingatia kikamilifu agizo hilo.

Hatua hiyo inatarajiwa kuwa sehemu ya mabadiliko katika mfumo wa usafiri wa Mabasi ya masafa marefu jijini Dar es Salaam, huku Serikali ikilenga kuhakikisha mabasi makubwa yanafanya shughuli zake katika vituo vilivyotengwa na abiria wanapata huduma rahisi na salama za usafiri wa ndani kuelekea wanakokwenda.



FARIDA SAID, MOROGORO 

Ng'ombe 56 waliokuwa mali ya mfugaji Clement Bernad sasa wamebaki kuwa sehemu ya historia yake ya ufugaji, ukame unaochochewa na mabadiliko ya tabianchi na kupungua kwa malisho vimemlazimisha kubadili mfumo wa ufugaji, akipunguza idadi ya mifugo na kuanza kuangalia zaidi uwezo wa kuzalisha malisho na kuihudumia mifugo aliyonayo.

Bernad mkazi wa kijiji cha Mtanana wilayani Kongwa Mkoa wa Dodoma ni mfano wa mabadiliko yanayowakabili wafugaji katika eneo hilo, uhaba wa malisho unalazimisha mifugo kutafuta chakula nje ya maeneo ya wafugaji na wakati mwingine kuingia katika mashamba ya wakulima, hali inayochochea migogoro kati ya pande hizo mbili.

Bernad anasema baada ya kupata elimu kutoka kwa wataalam kutoka Chuo kikuu cha Sokoine cha kilimo ( SUA ) kuhusu ufugaji unaozingatia mabadiliko ya tabianchi, ameamua kupunguza idadi ya ng'ombe wake na kubaki na idadi anayoamini anaweza kuihudumia kwa malisho na rasilimali alizonazo.

"Nilikuwa na ng'ombe 56 wa kienyeji, lakini baada ya kupata elimu nimeona umuhimu wa kuwa na mifugo ambayo ninaweza kuihudumia vizuri badala ya kuwa na mifugo mingi ambayo inakosa chakula," anasema Bernad.

Uamuzi huo unaakisi changamoto kubwa inayowakabili wafugaji nchini ambapo mabadiliko ya tabianchi yamekuwa yakibadilisha upatikanaji wa malisho na maji, hali inayogusa moja kwa moja uzalishaji wa mifugo ikiwemo maziwa.

Afisa Ugani wa Kata ya Mtanana Dominica Samweli Swai, anasema mabadiliko ya tabianchi yamekuwa miongoni mwa sababu zinazoendelea kuchochea migogoro kati ya wakulima na wafugaji kwasababau wafugaji wakikosa malisho wanalazimika kuuingiza mifugo kwenye mashamba ya wakulima.

Anasema suluhisho mojawapo ni kuwahamasisha wafugaji kuanza kuzalisha malisho katika maeneo yao ili kupunguza utegemezi wa malisho ya asili na ulazima wa kupeleka mifugo kutafuta chakula maeneo mengine.

"Wafugaji wengi wamehamasika kupanda malisho katika maeneo yao. Kama wafugaji watabadilika na kuacha mfumo wa kuchunga mifugo yao bila kuwa na uhakika wa malisho, tunaweza kupunguza migogoro mingi kati ya wakulima na wafugaji," anasema Swai.

Kata ya Mtanana pekee wafugaji 1,320 wenye jumla ya mifugo 7,829, idadi inayoweka wazi ukubwa wa mahitaji ya malisho katika eneo ambalo linakabiliwa na changamoto ya ukame.

Hata hivyo, kupanda malisho pekee kunaweza kusiwe jibu la muda mrefu iwapo aina ya malisho inayotumika haiwezi kustahimili vipindi virefu vya ukame.

Hapo ndipo watafiti kutoka Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) wameingia kazini kutafuta aina za malisho zinazoweza kustahimili ukame, huku wakilenga kutoa suluhisho linaloweza kuwasaidia wafugaji kuendelea kuzalisha mifugo hata katika mazingira yanayobadilika kutokana na mabadiliko ya tabianchi.

Akizungmza na waandishi wa habari Mkuu wa mradi kutoka Idara ya sayansi za wanyama, ufugaji viumbe maji na nyanda za malisho Chuo kikuu SUA, Prof. Sebastian Chenyambaga amesema utafiti huo ni sehemu ya mradi unaolenga kuimarisha uwezo wa wafugaji kustahimili na kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi, unaofadhiliwa na Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH).

Mradi huo wa miaka mitatu ulianza Oktoba 2025 na unatarajiwa kukamilika mwaka 2028, ukiangalia namna mabadiliko ya tabianchi yanavyowaathiri wafugaji na kutafuta mbinu zinazoweza kuongeza uwezo wao wa kukabiliana na athari hizo.

Mradi unatekelezwa katika Wilaya ya Kongwa mkoani Dodoma, Kishapu mkoani Shinyanga na Miatu mkoani Simiyu, maeneo ambayo yamechaguliwa katika utekelezaji wa utafiti huo.

Kwa upande wake Mtafiti kutoka Idara ya sayansi za wanyama, ufugaji viumbe maji na nyanda za malisho Chuo kikuu SUA, Dkt. Doris Lutatenekwa amesema utafiti pia unaenda sambamba na kupima aina za malisho zinazostahimili ukame.

Lengo la utafiti huo si kutafuta malisho ya kuokoa mifugo pekee, bali pia kuangalia namna wafugaji wanavyoweza kuendelea kuzalisha maziwa na bidhaa nyingine za mifugo katika mazingira yenye changamoto ya ukame.

Mkurugenzi wa Costech Dkt. Amos Nungu anasema mradi huo ni miongoni mwa hatua zinazolenga kutekeleza Dira ya Tanzania ya 2050 kwa kutumia sayansi, teknolojia na ubunifu katika kutatua changamoto zinazoikabili jamii.

Anasema tafiti zinazolenga kupata suluhisho la changamoto za mabadiliko ya tabianchi ni muhimu katika kujenga jamii yenye uwezo wa kustahimili mabadiliko ya mazingira na kulinda shughuli za kiuchumi za wananchi.

Kwa wafugaji kama Bernad, mabadiliko hayo hayapo tena kwenye vitabu au mijadala ya wataalamu, yameingia moja kwa moja katika maisha yao yakimlazimisha mfugaji kujiuliza si tu “nitafuga ng'ombe wangapi?”, bali pia “nitawapataje chakula wakati mvua hazitoshelezi?”









Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, akizungumza na viongozi wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), Ikulu Chamwino, mkoani Dodoma, tarehe 10 Agosti, 2026.




Katibu NEC Itikadi, Uenezi na Mafunzo, Ndugu Kenani Kihongosi amesisitiza kuwa  Vijana ndio walinda Nchi hivyo wanatakiwa kuilinda amani ya nchi ili waweze kufanya shughuli za uzalishaji kwa maendeleo ya Taifa na familia zao.

Ndugu Kenani ameyasema hayo leo tarehe 10 Agosti 2026 wakati akitoa mada kwenye Mafunzo ya Uongozi wa Seneti za Vyuo vya Kati na Vyuo Vikuu yanayofanyika katika Chuo cha Mafunzo Ihemi mkoani Iringa.

Pia, ametumia jukwaa hilo kukemea lugha chafu zinazotolewa kwa Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan katika mitandao ya kijamii na kuwasihi vijana kuwa mstari wa mbele kumtetea Rais na wasikae kimya.

Aidha ametoa wito kwa Vijana wa Chama cha Mapinduzi  ndani na nje ya Tanzania kulipa Ada ya uanachama akieleza uhai wa Chama cha Mapinduzi (CCM) unatokana na wanachama kulipia ada.












Na Victor Masangu, Kibaha

Mwenyekiti wa Jumuiya ya wawake (UWT) Wilaya ya Kibahaa mjini Elina Mgonja Katika kuuunga juhudi za Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuwakomboa wanawake kiuchumi ameamua kutoa mafunzo ya ujasiriamali kwa vitendo kwa wanawake wapatao 400 wa Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha Mkoa wa Pwani kwa lengo la kuondokana na wimbi la umasikini.

Akizungumza katika ziara yake maaalumu ya kikazi yenye lengo la kuwatembelea wanawake wa (UWT) katika kata mbali mbali kwa ajili ya kuwapa maarifa na ujuzi na kujifunza jinsi ya kutengeneza bidhaa za aina tofauti ambazo zitawapa fursa ya kujiajiri wao wenyewe na kuondokana na kuwa tegemezi kila kukicha.

Elina amebainisha kuwa amefanya ziara hiyo ikiwa ni utekelezaji wa ahadi yake ambayo aliitoa ya kuwasaidia wanawake wa UWT kutoka kata zote 14 zilizopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha na kwamba mafunzo hayo ambayo ameamua kuyatoa bure bila malipo yoyote yatakuwa ni mkombozi mkubwa katika kujikwamua kiuchumi,

Nao baadhi ya wanawake ambao wamepata mafunzo hayo akiwemo Mwajuma Makuka wamesema kwamba maffunnzo hayo yataweza kuwasaidia kwa kiasi kikubwa kuondokana na kuwa tegemezi na kwamba watakwenda kuyafanyia kazi kwa hali na mali kwa lengo la kuweza kuondokana na wimbi la umasikini.

"Kwa kweli tunapenda kumshukuru kwa dhati Mwenyekiti wetu wa UWT Wilaya ya Kibaha mjini Elina Mgonjwa kwa kuweza kufanya ziara hii na kuja kutupa elimu na mafunzo ya ujasiliamali na tumeweza kujifunza mambo mbali mbali ikiwemo kutengeneza bidhaa kama vile kutengeneza batiki, sabuni za kufulia, sabuni za kuogea pamoja na kupata ujuzi ambao tutakwenda kuufanyia kazi katika kutekeleza majukumu yetu,"amebainisha Mwajuma.

Mwenyekiti huyo wa UWT anaendelea na ziara yake ya kikazi ambapo hadi sasa ameshatembelea kata 7 ambazo ni Msangani, Mkuza, Tumbi, Maili moja, Kongowe, Kibaha pamoja na Kata ya Misususugu ambapo jumla ya wanawake 400 wameweza kunufaika na mafunzo hayo ya ujasiriamali kwa vitendo.









Na. Jordan Mbwambo, WF, Dodoma.

Wizara ya Fedha kwa kushirikiana na Taasisi ya Saratani Ocean Road imeanza kutekeleza zoezi la utoaji wa elimu kuhusu saratani pamoja na vipimo vya uchunguzi wa awali wa saratani kwa watumishi wa Wizara hiyo ili kuongeza uelewa wa namna ya kujikinga, kutambua dalili za awali na kuchukua hatua stahiki kukabiliana na ugonjwa huo.

Zoezi hilo litakalohusisha utoaji wa elimu kuhusu saratani mbalimbali, ikiwemo saratani ya matiti, tezi dume na shingo ya kizazi, pamoja na vipimo vya awali linatarajiwa kufanyika kuanzia tarehe 10 hadi 14 Agosti 2026, katika Ofisi za Wizara ya Fedha, Mtumba, jijini Dodoma.

Akizungumza wakati akifungua mafunzo hayo, Mkurugenzi wa Usimamizi wa Mali za Serikali, Wizara ya Fedha, Bw. Chotto Sendo, alisema ni muhimu kwa watumishi kufuatilia elimu ya afya ya saratani ili kuwa na uelewa wa kutosha kukabiliana na ugonjwa huo.

‘‘Ni muhimu kuwa na uelewa sahihi kuhusu saratani, hususan kwa kuzingatia kwamba utambuzi wa ugonjwa huo katika hatua za awali una nafasi kubwa katika matibabu na kuokoa maisha’’’ Alisema Bw. Sendo.

Aliwasisitiza watumishi wa Wizara hiyo kutumia fursa hiyo kupata elimu pamoja na kufanya vipimo vya awali vinavyotolewa ili kufahamu hali zao za afya.

Kwa upande wake Daktari Bingwa wa Saratani, Taasisi ya Saratani Ocean Road, Dkt. Frank Ruta, aliwahimiza watumishi hao kutopuuza mabadiliko au dalili zisizo za kawaida katika miili yao na kufika katika vituo vya afya kwa ajili ya uchunguzi na ushauri wa kitaalamu.

Alisema utambuzi wa saratani katika hatua za awali unaongeza nafasi ya mafanikio ya matibabu, hivyo jamii inapaswa kujenga utamaduni wa kufanya uchunguzi wa afya mara kwa mara na kuchukua hatua za mapema katika kuzuia na kukabiliana na saratani.

Dkt. Ruta alisemna elimu hiyo ni sehemu ya jitihada za kuimarisha uelewa wa watumishi na jamii kwa ujumla kuhusu afya na kuwahamasisha kuchukua hatua za mapema katika kuzuia na kukabiliana na saratani.

Mkurugenzi wa Idara ya Usimamizi wa Mali za Serikali, Wizara ya Fedha, Bw. Chotto Sendo, akizungumza katika zoezi la utoaji wa elimu kuhusu saratani pamoja na vipimo vya uchunguzi wa awali wa saratani kwa watumishi wa wizara hiyo, linalofanyika katika Ofisi za Wizara ya Fedha, Mtumba, jijini Dodoma, kuanzia tarehe 10 hadi 14 Agosti 2026.

Afisa Utumishi Mwandamizi, Wizara ya Fedha, Bw. Salum Said, akifafanua jambo katika zoezi la utoaji wa elimu kuhusu saratani pamoja na vipimo vya uchunguzi wa awali wa saratani kwa watumishi wa Wizara hiyo, linalofanyika katika Ofisi za Wizara ya Fedha, Mtumba, jijini Dodoma, kuanzia tarehe 10 hadi 14 Agosti 2026.




Daktari Bingwa wa Saratani kutoka Taasisi ya Saratani Ocean Road, Dkt. Frank Ruta, akitoa elimu kuhusu kinga, utambuzi na matibabu ya saratani kwa watumishi wa Wizara ya Fedha, katika zoezi linalofanyika katika Ofisi za Wizara ya Fedha, Mtumba, jijini Dodoma, kuanzia tarehe 10 hadi 14 Agosti 2026.



Baadhi ya Watumishi wa Wizara ya Fedha wakifuatilia elimu iliyokuwa inatolewa na wataalamu kutoka Taasisi ya Saratani Ocean Road, kuhusu namna ya kujikinga, kutambua dalili za awali na kuchukua hatua stahiki katika kukabiliana na ugonjwa wa saratani, katika zoezi linalofanyika katika Ofisi za Wizara ya Fedha, Mtumba, jijini Dodoma, kuanzia tarehe 10 hadi 14 Agosti 2026.


(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, WF, Dodoma)

 Na. Josephine Majura na Asia Singano, WF – Dodoma.


Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), amesema Serikali itaendelea kuimarisha mifumo ya bajeti na usimamizi wa fedha za umma kwa kuzingatia usawa wa kijinsia, hatua inayolenga kuhakikisha rasilimali za Serikali zinatumika kwa ufanisi katika kuchochea maendeleo jumuishi.

Mhe. Balozi Omar (Mb), aliyasema hayo jijini Dodoma, alipokutana na kufanya mazungumzo na Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Usawa wa Kijinsia na Uwezeshaji wa Wanawake (UN Women), nchini Tanzania, Bi. Julia Broussard, katika Ukumbi wa Mikutano wa Waziri wa Fedha, Treasury Square jijini Dodoma.

Mazungumzo hayo yalilenga kuimarisha ushirikiano wa kimkakati kati ya Wizara ya Fedha na UN Women, hususani katika utekelezaji wa Bajeti inayozingatia Masuala ya Kijinsia (Gender-Responsive Budgeting – GRB).

‘’Serikali ya Tanzania, inatambua umuhimu wa kuzingatia masuala ya kijinsia katika sera za fedha, mchakato wa uandaaji wa bajeti, ugawaji wa rasilimali na ufuatiliaji wa utekelezaji wa programu za Serikali ili kuhakikisha mipango ya kitaifa inachangia katika kujenga uchumi jumuishi na wenye usawa’’ alisema Mhe. Balozi Omar (Mb).

Alisema Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2026/2027, imezingatia usawa wa jinsia huku Serikali ikiona umuhimu wa kuandaa Taarifa Maalum ya Bajeti inayozingatia Masuala ya Kijinsia (Gender Budget Statement) kama sehemu ya mfumo rasmi wa usimamizi wa fedha za umma.

Alibainisha kuwa hatua hiyo inaweka msingi wa kuimarisha Mfumo wa Uandaaji wa Bajeti Unaozingatia Masuala ya Kijinsia (GRB), utakaosaidia kuhakikisha masuala ya kijinsia yanaingizwa kikamilifu katika mipango, uandaaji wa bajeti, ugawaji wa rasilimali na ufuatiliaji wa utekelezaji wa programu za umma.

“Muhimu siyo tu kuangalia kiasi cha fedha kilichotengwa au kutumika, bali pia matokeo yanayopatikana kutokana na rasilimali hizo na kupima matokeo ya matumizi ya fedha za umma’’. Alisema Mhe. Balozi Omar (Mb).

Aliongeza kuwa, katika kuhakikisha rasilimali zinazotengwa kwa ajili ya usawa wa kijinsia na uwezeshaji wa wanawake zinafuatiliwa kwa ufanisi, mfumo wa Gender Budget Tagging unaopangwa kuanzishwa utakuwa nyenzo muhimu ya kubaini, kufuatilia na kuchambua matumizi ya bajeti yanayolenga masuala hayo.

Kwa upande wake, Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Usawa wa Kijinsia na Uwezeshaji wa Wanawake (UN Women), nchini Tanzania, Bi. Julia Broussard alisema Wizara ya Fedha ina nafasi muhimu katika kuhakikisha Tanzania inapata na kutoa taarifa zinazohitajika kuhusu Kiashiria cha 5.c.1 cha Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDG 5), kinachopima uwepo wa mifumo ya kufuatilia na kuweka wazi mgao na matumizi ya rasilimali za umma kwa ajili ya kukuza usawa wa kijinsia na uwezeshaji wa wanawake.

Alisema Shirika hilo litaendelea kushirikiana na Wizara ya Fedha, katika kuimarisha mifumo na uwezo wa kitaasisi unaohitajika ili kuhakikisha masuala ya kijinsia yanaingizwa kikamilifu katika mipango, bajeti na usimamizi wa rasilimali za umma.

Ushirikiano huo unalenga kuimarisha matumizi ya takwimu na taarifa za bajeti katika kufanya maamuzi, kufuatilia rasilimali zinazotengwa kwa masuala ya kijinsia na hatimaye kuhakikisha matumizi ya fedha za umma yanaongeza matokeo chanya kwa wananchi, hususan katika kukuza usawa wa kijinsia na uwezeshaji wa wanawake.

Kikao hicho pia kilihudhuriwa na viongozi Mbalimbali wa Wizara ya Fedha, akiwemo Kamishna Msaidizi, Idara ya Fedha za Nje, Bw. Melckzedek Mbise, Kamishna Msaidizi Idara ya Usimamizi wa Bajeti ya Serikali, Bw. Andambike Mololo pamoja na Wataalamu wengine wa Wizara ya Fedha.
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akiagana na Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Usawa wa Kijinsia na Uwezeshaji wa Wanawake (UN Women), nchini Tanzania, Bi. Julia Broussard, baada ya kumalizika kikao cha Waziri wa Fedha na Ujumbe kutoka Shirika hilo, kilichofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Waziri, Treasury Square jijini Dodoma.
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akiongoza Kikao chake na Ujumbe kutoka Shirika la Umoja wa Mataifa la Usawa wa Kijinsia na Uwezeshaji wa Wanawake (UN Women), Ukiongozwa na Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Usawa wa Kijinsia na Uwezeshaji wa Wanawake (UN Women), nchini Tanzania, Bi. Julia Broussard, ulipomtembelea Ofisini kwake, Treasury Square jijini Dodoma.
Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Usawa wa Kijinsia na Uwezeshaji wa Wanawake (UN Women), nchini Tanzania, Bi. Julia Broussard, akizungumza wakati wa kikao na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), hayupo pichani, alipomtembelea Ofisini kwake, Treasury Square jijini Dodoma.
Kikao cha Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), na Ujumbe wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Usawa wa Kijinsia na Uwezeshaji wa Wanawake (UN Women), nchini Tanzania katika Ukumbi wa Mikutano wa Waziri wa Fedha, Treasury Square jijini Dodoma.
Kamishna Msaidizi, Idara ya Fedha za Nje, Bw. Melckzedek Mbise, (wakwanza kushoto), Kamishna Msaidizi Idara ya Usimamizi wa Bajeti ya Serikali, Bw. Andambike Mololo, (wapili kushoto) pamoja na Wataalamu wengine wa Wizara ya Fedha, wakifuatilia kikao cha Mhe. Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), hayupo pichani, na Ujumbe wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Usawa wa Kijinsia na Uwezeshaji wa Wanawake (UN Women), nchini Tanzania, kilichofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Waziri, Treasury Square jijini Dpodoma.
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), (watano kulia), akiwa katika picha ya pamoja na Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Usawa wa Kijinsia na Uwezeshaji wa Wanawake (UN Women), nchini Tanzania, Bi. Julia Broussard, (watano kushoto), Kamishna Msaidizi, Idara ya Fedha za Nje, Bw. Melckzedek Mbise, (watatu kulia), Kamishna Msaidizi Idara ya Usimamizi wa Bajeti ya Serikali, Bw. Andambike Mololo (wa kwanza kulia), Wataalamu kutoka Wizara ya Fedha, pamoja na wajumbe kutoka UN Women, baada ya kumalizika kikao cha Mhe. Balozi Omar (Mb) na Ujumbe huo.

(Picha na Kitengo Cha Mawasiliano Serikalini, WF - Dodoma)


Top News