
Na. Sgt. Geofrey Jacka - DODOMA
Kamishna wa Sheria na Uendeshaji wa Magereza, CP. Nicodemus Tenga, kwa niaba ya Mkuu wa Jeshi la Magereza Tanzania, CGP. Jeremiah Yoram Katungu, Mei 19, 2026 amefungua Mafunzo ya Mfumo wa Usimamizi wa Mali za Kudumu za Serikali (GAMIS), akieleza kuwa kufanyika kwa mafunzo hayo ni utekelezaji wa Maagizo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.
CP. Tenga amesema, katika kuhitimisha Mafunzo ya Uongozi kwa Maafisa Magereza, Mei 9, 2026 Ukonga Dar Es Salaam, Rais Dkt. Samia, aliekeleza Jeshi la Magereza kutumia TEHAMA katika utendaji wake ili kuongeza ufanisi na uwazi serikalini na kuendana na kasi ya mabadiliko ya Teknolojia.
Aidha, CP. Tenga, amesema ni matarajio ya Jeshi baada ya mafunzo hayo, wataalamu wa ununuzi watakuwa na maarifa mapya ya kutumia mfumo wa GAMIS na kuwaongezea uelewa wa Sheria na Kanuni za usimamizi wa mali za kudumu za Serikali, kuongeza uwajibikaji, kuboresha utunzaji wa kumbukumbu na kuimarisha usimamizi wa rasilimali za Serikali ikiwemo uhamishaji, uazimishaji na uondoshaji wa mali.
"Ndugu washiriki, majukumu ya ugavi ni mhimili muhimu katika utendaji wa Jeshi, ufanisi wa kazi zenu una mchango mkubwa katika kuhakikisha upatikanaji wa vifaa na huduma muhimu kwa wakati, uwazi na kwa kuzingatia thamani ya fedha, hivyo niwatake muwe makini wakati wote wa mafunzo ili yaweze kuwa na tija" alisema CP. Tenga
Akitoa taarifa ya mafunzo, Mkuu wa Kitengo cha Ununuzi Jeshi la Magereza, ACP Henry Masawe amesema, Jeshi la Magereza lina jukumu la kutunza na kuhifadhi vifaa na mali zote za kudumu kwa ufanisi na kufuatilia utunzaji sahihi wa kumbukumbu zake hadi pale zitakapo ondoshwa.
Aidha ACP. Masawe, amesema lengo la mafunzo hayo ni kuwawezesha wagavi kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao kufuatilia na kusimamia mali zote za kudumu za Serikali kwa kutumia mfumo.
Mafunzo hayo ya siku nne ya GAMIS, yanafanyika katika Ukumbi wa Rugimbana jijini Dodoma, yakiweka msisitizo kuwa matumizi ya mifumo ya kisasa ni sehemu muhimu ya kuimarisha uwajibikaji, uwazi na ufanisi katika utendaji wa Jeshi la Magereza.

Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dkt. Rhimo Nyansaho, ameieleza Bunge kuwa hali ya usalama katika mipaka ya nchi imeendelea kuwa shwari na yenye utulivu katika kipindi cha mwaka wa fedha 2025/26, huku vyombo vya ulinzi vikiendelea kuchukua hatua madhubuti kuhakikisha ulinzi wa taifa unaimarika zaidi.
Akizungumza wakati akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa mwaka wa fedha 2026/27, Waziri huyo amesema Tanzania ina jumla ya kilomita 5,923.41 za mipaka, inayojumuisha mipaka ya nchi kavu, anga pamoja na eneo la maji.
Kwa mujibu wa Waziri Nyansaho, mipaka ya nchi kavu ya Tanzania inagusa mataifa ya Burundi, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Kenya, Malawi, Msumbiji, Rwanda, Uganda na Zambia, huku upande wa bahari ya Hindi Tanzania ikipakana na visiwa vya Comoro na Shelisheli.
Ameeleza kuwa katika kipindi hicho hakujakuwa na matukio yoyote makubwa yaliyoashiria uvunjifu wa amani kati ya Tanzania na nchi jirani, jambo linaloonesha uimara wa diplomasia na ulinzi wa mipaka ya taifa.
Hata hivyo, Waziri Nyansaho amesema bado kuna changamoto kadhaa za kiulinzi na kiusalama katika baadhi ya maeneo ya mipaka, ikiwemo uharibifu wa alama za mipaka, ukosefu wa miundombinu ya barabara za ulinzi katika baadhi ya maeneo, pamoja na uharibifu wa baadhi ya miundombinu hiyo iliyopo.
Aidha, amebainisha kuwa baadhi ya changamoto zinatokana na hali ya ndani ya nchi jirani zinazopakana na Tanzania, jambo linalohitaji ufuatiliaji wa karibu na ushirikiano wa kikanda katika kuhakikisha usalama unaendelea kudumishwa.
Waziri huyo ameihakikishia Bunge kuwa Serikali kupitia vyombo vya ulinzi na usalama itaendelea kuimarisha ulinzi katika mipaka yote ya nchi kwa lengo la kulinda raia, mali zao na maslahi ya taifa kwa ujumla.
Waziri wa Katiba na Sheria, Dkt.Juma Homera amesema serikali imechoshwa na tabia ya baadhi ya watu kutumia mitandao ya kijamii kueneza matusi, uchochezi na taarifa zisizo na ukweli dhidi ya serikali na viongozi wake.
Akifungua mafunzo ya siku tatu kwa mawakili wa serikali yaliyofanyika jijini Arusha, Dk Homera amesema tayari orodha ya watu wanaotuhumiwa kujihusisha na vitendo hivyo imewasilishwa Wizara ya Mambo ya Ndani kwa ajili ya hatua zaidi za kisheria kupitia Jeshi la Polisi.
Kauli hiyo imeungwa mkono na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Damas Ndumbaro ambaye alisisitiza umuhimu wa mawakili wa serikali kushiriki kikamilifu kupambana na upotoshaji unaofanyika mtandaoni.
“Uhuru wa kutoa maoni upo, lakini usitumike kuvunja sheria, kuchochea vurugu au kudhalilisha wengine,” amesema Dk Homera.
Hatua hiyo inaelezwa kuwa sehemu ya juhudi za serikali kuhakikisha matumizi ya mitandao yanafuata maadili, sheria na kulinda amani ya nchi.
Na Janeth Raphael MichuziTv- Bungeni Dodoma
Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Rhimo Nyansaho, ameainisha vipaumbele nane vitakavyoongoza utekelezaji wa shughuli za Wizara ya Ulinzi katika mwaka wa fedha 2026/27, vikilenga kuimarisha uwezo wa kiulinzi, kuendeleza Jeshi, pamoja na kuhakikisha usalama wa Taifa unaimarishwa kwa kiwango cha juu zaidi.
Akiwasilisha bungeni jijini Dodoma makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara hiyo, Dkt. Nyansaho amesema Serikali imeweka mkazo katika kuboresha na kuimarisha Jeshi la Ulinzi kwa kulipatia zana na vifaa vya kisasa vya kijeshi, teknolojia ya kisasa ya mawasiliano pamoja na kuendeleza rasilimali watu ili kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yake ya msingi.
Amefafanua kuwa hatua hiyo inalenga kuhakikisha Jeshi linakuwa na uwezo wa kukabiliana na changamoto za kiusalama za sasa na zijazo, ambazo zinabadilika kwa kasi kutokana na maendeleo ya teknolojia na mazingira ya kikanda na kimataifa.
Katika upande wa ustawi wa wanajeshi, Waziri huyo amesema Serikali itaendelea kuboresha mazingira ya kazi kwa wanajeshi kupitia matunzo bora ya vifaa na zana za kijeshi, mafunzo ya mara kwa mara, pamoja na mazoezi ya kijeshi yenye kuendana na viwango vya kimataifa.
Aidha, amebainisha kuwa huduma za afya, makazi na maslahi ya wanajeshi kwa ujumla pia yataendelea kupewa kipaumbele ili kuongeza morali, nidhamu na ufanisi katika utendaji kazi wa vyombo vya ulinzi na usalama.
Kuhusu Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), Dkt. Nyansaho amesema Serikali imejipanga kuongeza uwezo wa jeshi hilo kwa kuboresha miundombinu yake ili kuwezesha vijana wengi zaidi kupata fursa ya mafunzo ya awali ya kijeshi sambamba na stadi mbalimbali za kazi zitakazowawezesha kujitegemea baada ya mafunzo.
Ameongeza kuwa hatua hiyo ni sehemu ya mkakati mpana wa Serikali wa kuwawezesha vijana kiuchumi, kijamii na kiulinzi, huku JKT likiendelea kuwa chombo muhimu katika malezi ya uzalendo na nidhamu kwa vijana wa Kitanzania.
Katika kuimarisha ulinzi wa Taifa, Waziri Nyansaho pia amesema Jeshi la Akiba litaendelea kuimarishwa ili kuongeza utayari wake wa kushiriki katika ulinzi wa nchi pale litakapohitajika, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kuongeza uwezo wa kiulinzi wa ndani.
Aidha, Wizara hiyo itaendelea kulinda na kuendeleza miradi ya kimkakati ya Taifa ili kuhakikisha inatoa mchango chanya katika maendeleo ya kiuchumi na kijamii ya nchi.
Pamoja na hayo, Serikali itaendelea kuboresha taasisi na mashirika yanayojihusisha na utafiti wa masuala ya kijeshi, sambamba na kuanzisha viwanda vipya vya ulinzi vitakavyozalisha bidhaa za kijeshi na kiraia kwa kushirikiana na sekta binafsi.
Kwa mujibu wa Dkt. Nyansaho, hatua hiyo inalenga kupunguza utegemezi wa bidhaa za ulinzi kutoka nje ya nchi na kuimarisha uwezo wa ndani wa uzalishaji wa teknolojia na vifaa vya kiulinzi.
Kuhusu ushirikiano wa kimataifa, amesema Tanzania itaendelea kushirikiana na Umoja wa Mataifa, Umoja wa Afrika (AU), Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) pamoja na mataifa mbalimbali duniani katika masuala ya ulinzi na usalama.
Ameongeza kuwa ushirikiano huo ni muhimu katika kukabiliana na changamoto za kiusalama za kikanda na kimataifa, ikiwemo ugaidi, uhalifu wa kimataifa na majanga ya kibinadamu.
Aidha, Wizara ya Ulinzi itaendelea kushirikiana kwa karibu na mamlaka za kiraia katika kukabiliana na majanga na dharura mbalimbali pale yanapotokea, ikiwa ni sehemu ya kuimarisha usalama na ustawi wa wananchi.
Kwa ujumla, vipaumbele vilivyoainishwa na Wizara hiyo vinaonesha dhamira ya Serikali ya kuendelea kuimarisha Jeshi la Ulinzi, kukuza uwezo wa Jeshi la Kujenga Taifa, pamoja na kuhakikisha Tanzania inaendelea kuwa na mazingira salama na imara kwa maendeleo ya Taifa kwa ujumla.

Taasisi ya Saratani Ocean Road, imeanza kutoa huduma bora za kisasa kwa kutumia mtambo wa tiba mionzi ya nyuklia kwa wagonjwa wa saratani.
Daktari Bingwa wa Tiba Mionzi ya Nyuklia wa taasisi hiyo, Tausi Maftaha, amesema wameanza kutoa matibabu kwa kutumia mtambo huo wa kisasa ambao una uwezo wa kuelekeza tiba na kutengeneza dawa za saratani.
Amesema mtambo huo una uwezo wa kutengeneza dawa, ambazo awali walikuwa waagiza kutoka Ulaya na Afrika Kusini.
"Tulikuwa tunaagiza dawa kutoka katika nchi zilizoendelea pamoja na Afrika Kusini, lakini kutokana aina hizi za dawa haziishi muda mrefu yaani huwezi kuweka kama za kawaida maabara au Famasi, hizi ni dawa ambazo unatengeneza katika mtambo, ikishatengenezwa inatakiwa mgonjwa atumie hapo hapo", amesema.
Dk. Tausi amesema serikali kwa kuona hilo, ikaamua kufanya uwekazaji mkubwa wa kuwa na mtambo huo na taasisi ndiyo itakuwa kituo kikuu cha kusambaza dawa hizo katika hospitali nyingine na nchi jirani.
Amesema dawa zinazotengeneza zinachunguza aina zote za saratani ispokuwa saratani ya damu ambayo mfumo wake tofauti.
Aidha Dk. Tausi amesema dawa hizo zinafaida nyingi zikiwemo mgonjwa kupewa dawa sahihi, inafupisha muda wa matibabu, inaokoa gharama kwa wagonjwa kwasababu dawa za saratani gharama zake ziko juu.
Pia amesema mitambo hiyo ya kisasa ndiyo inayotumika kutoa matibabu ya saratani katika nchi ziliendelea na umefungwa na kampuni ya kimataifa.
"Ni utaalamu wa kisasa ukienda, Ulaya, India, Afrika Kusini utaikuta mitambo hii, kwahiyo huduma tunayotoa hapa ndiyo hiyo hiyo inayitolewa nchi za nje, hivyo hakuna sababu ya mgonjwa kwenda kupata huduma hiyo nje ya nchi, labda kama mahitaji binafsi", amesema.
Dk. Tausi amemshukuru Rais Dk. Samia kwasababu aliaanza na mradi huu tangu akiwa Makamu wa Rais na ametoa fedha hadi sasa umekamilika, ameokoa fedha nyingi.
Aidha Dk. Tausi amewataka wananchi kutokuwa na hofu ya kuwa mionzi nyukilia ina madhara, alisema mionzi hiyo ni tiba na kwamba wananchi wawe na utaratibu wa kufika mapema katika hospitali kupata huduma kabla matatizo hayajawa makubwa.
Amesema waondokane na dhana potofu kwamba mwenye saratani akifanyiwa upasuaji huwa wanapoteza maisha, upasuaji moja ya tiba kuhakikisa mgonjwa anapona.
Dk. Tausi amesema mgonjwa wa saratani akiwahi kupata matibabu mapema anapona kabisa.
Mageuzi ya biashara ya mazao nchini yanaendelea kushuhudiwa kupitia ushirikiano kati ya COPRA na Bodi ya Stakabadhi za Ghala (WRRB).
Akizungumza katika warsha kuelekea kilele cha maadhimisho ya miaka 20 ya WRRB, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Nafaka na Mazao Mchanganyiko (COPRA), Bi. Irene Mlola, amesema matumizi ya mfumo wa mauzo kidijitali unaojumuisha Mfumo wa Stakabadhi Ghalani yameendelea kurahisisha biashara ya mazao, kuongeza fursa za masoko na kunufaisha wadau mbalimbali katika mnyororo wa thamani.
Mafanikio mengine yaliyochagizwa na COPRA kupitia mfumo huo ni pamoja na;
Kuongezeka kwa bei ya mazao kwa wakulima kwa wastani wa asilimia 15 - 30, Wakulima kunufaika na asilimia 75 hadi 80 ya bei ya soko la dunia kwa mazao mbalimbali, Kuongezeka kwa uzalishaji wa baadhi ya mazao kwa zaidi ya asilimia 30, Kuongezeka kwa thamani ya biashara ya mazao kutoka shilingi bilioni 896 hadi trilioni 1.4, asilimia 94 ya mapato ya mazao ya mbaazi, choroko, dengu na ufuta kwenda moja kwa moja kwa wakulima.
Bi. Mlola ameeleza mafanikio mengine ni kuongezeka kwa mapato ya kodi katika sekta ya kilimo kutoka shilingi bilioni 26 hadi bilioni 40, kupanuka kwa masoko ya kimataifa pamoja na kuongezeka kwa matumizi ya minada ya kidijitali na huduma za kifedha kwa wakulima.
Aidha, Bi. Mlola ameipongeza WRRB kwa kuadhimisha miaka 20 ya huduma na kuahidi kuendeleza ushirikiano kati ya taasisi hizo mbili.
-Magereza 12 Morogoro Yanufaika na Mradi wa Nishati Safi ya Kupikia kutoka REA
Jeshi la Magereza Mkoa wa Morogoro limeendelea kuhamasishwa matumizi ya nishati safi ya kupikia ikiwa ni sehemu ya Mkakati wa Serikali kuhakikisha Asilimia 80 ya wanatumia wahamie kutumia nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034.
Akizungumza wakati wa ziara ya kukagua miradi ya nishati safi ya kupikia kwa Jeshi la Magereza mkoani Morogoro, Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB), Mhe. Balozi Meja Jenerali (Mstaafu), Jacob Kingu amesema kuwa lengo la taifa la kufikia matumizi makubwa ya nishati safi ya kupikia linawezekana kutokana na uwepo wa vyanzo mbalimbali vya nishati hiyo.
Amesema wananchi wana nafasi ya kuchagua aina ya nishati safi kulingana na mazingira wanayoishi, ikiwemo gesi, mkaa mbadala pamoja na matumizi ya umeme kwa ajili ya kupikia.
“Inawezekana ifikapo mwaka 2034 asilimia 80 ya watanzania wanatumia nishati safi za kupikia maana zipo nyingi" amesema Mwenyekiti Kingu.
Aidha, ameeleza kuwa Wakala wa Nishati Vijijini (REA) unaendelea kupeleka huduma ya umeme katika Vijiji na Vitongoji jambo litakalowezesha wananchi wengi zaidi kutumia umeme kama chanzo cha nishati safi ya kupikia.
Kwa upande wake, Mkuu wa Magereza Mkoa wa Morogoro, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Magereza (SACP), Peter Anatory amesema mradi wa majiko ya nishati safi ya kupikia unaotekelezwa na Wakala wa Nishati Vijijini (REA) umewezesha magereza 12 ya Mkoa wa Morogoro kunufaika na huduma hiyo.
Amesema kupitia mradi huo, magereza hayo yamepata majiko 15 yanayotumia mkaa rafiki kwa mazingira pamoja na tani 236 za mkaa huo, hali iliyosaidia kuongeza matumizi ya nishati safi katika taasisi za magereza.
“Mradi huu umekuwa kichocheo kikubwa kwa magereza katika kuhakikisha tunatumia nishati safi ya kupikia,” amesema Anatory.
Naye Kamishna Msaidizi wa Magereza (ACP) Samuel Aron Mwakatika amesema matumizi ya nishati safi yana mchango mkubwa katika kuboresha maisha ya wananchi, kulinda mazingira pamoja na kukuza uchumi wa taifa.
Amesema katika Chuo cha Udereva KPF Kingolwira, matumizi ya nishati safi yamesaidia kuokoa muda uliokuwa unapotea kwa wanafunzi kwenda kutafuta kuni.
“Katika chuo hiki tuna wanafunzi 381, hivyo zamani ilikuwa lazima kuwe na kundi la wanafunzi wanaokwenda kutafuta kuni jambo lililokuwa linapunguza muda wa kujifunza. Nishati safi imesaidia kuondoa changamoto hiyo,” amesema Mwakatika.
Aidha, Mrakibu Mwandamizi wa Magereza (SSP), Nicostatus Magori amesema gereza hilo liliacha kutumia kuni kwa ajili ya kupikia chakula cha wafungwa tangu Desemba mwaka 2024 baada ya kuanza kutekelezwa kwa mradi huo wa kufungiwa mifumo ya nishati safi ya kupikia katika magereza.
.jpeg)
Mkutano huo wa Kimataifa unawakutanisha pia wataalamu wa nishati, wawekezaji na mashirika ya kimataifa, ambapo utajadili matumizi ya nishati ya nyuklia kwa maendeleo ya Bara la Afrika. Mkutano huo pia unalenga kujadili namna bora ya kuongeza upatikanaji wa nishati ya umeme Afrika, kupunguza uchafuzi wa mazingira, kusaidia maendeleo ya viwanda, kukuza ubunifu wa teknolojia za nishati ya nyuklia pamoja na kuvutia wawekezaji katika miradi ya nishati
Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela imefanya ziara katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma kwa lengo la kujifunza namna ya utekelezaji wa miradi ya kimkakati ya maendeleo ili kuboresha ukusanyaji wa mapato, kuinua uchumi na kuboresha upatikanaji wa huduma kwa jamii.
Ziara hiyo ilihusisha madiwani pamoja na wataalamu kutoka Manispaa ya Ilemela waliotembelea miradi mbalimbali kwa ajili ya kujifunza mbinu za usimamizi na utekelezaji.
Akizungumza kuhusu miradi hiyo, Mchumi katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Mataso Ndege, alisema kuwa lengo la utekelezaji wa miradi hiyo ni kuongeza mapato ya halmashauri, kupunguza utegemezi kwa serikali kuu, kuvutia uwekezaji, kupendezesha jiji pamoja na kuongeza ajira na huduma kwa wananchi.
“Utekelezaji wa miradi ya kimkakati umegawanyika katika awamu tatu ambapo awamu ya kwanza imehusisha ujenzi wa Government City Complex (Mtumba Complex), Dodoma City Hotel pamoja na Soko la wazi la Machinga, ambayo yote imekamilika.
Awamu ya pili itahusisha miradi ya Nyerere Square Plaza na Nunge Investment Building, huku awamu ya tatu ikijumuisha Dodoma City Complex Mall, Dodoma City Complex Apartment na NK Complex” alisema Ndege.
Nae, Mtakwimu kutoka Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Nora Mulambo ya alisema kuwa mradi wa Dodoma City Hotel uligharimu shilingi bilioni 11.9, huku mradi wa Mtumba Complex unaojumuisha ukumbi wa mikutano unaotekelezwa kwa awamu tatu nao utagharimu jumla ya shilingi bilioni 59.
Alifafanua kuwa awamu ya kwanza ya mradi huo iligharimu shilingi bilioni 18 na mradi umekamilika kwa asilimia 99. Aidha, alisema kuwa ujenzi wa Soko la wazi la Machinga uligharimu shilingi bilioni 9.5 na manufaa ya miradi hiyo yanaonekana kutokana na makusanyo ya mapato.
Kwa upande wake, Naibu Meya wa Manispaa ya Ilemela, Kuruthum Abdallah alisema kuwa ziara hiyo imelenga kupata uzoefu na mbinu zinazotumiwa na Halmashauri ya Jiji la Dodoma katika kusimamia miradi ya maendeleo.
“Tumekuja kujifunza na kubadilishana uzoefu ili kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo na utoaji wa huduma bora kwa wananchi” alisema Abdallah.
Ziara hiyo inatarajiwa kuimarisha ushirikiano kati ya halmashauri hizo mbili pamoja na kuongeza uwezo wa kiutendaji katika kusimamia na kutekeleza miradi ya maendeleo yenye tija kwa wananchi.



.jpeg)
.jpeg)


.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)

















.jpeg)


.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)



.jpeg)
.jpeg)





