Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga (Mbinga DC) Joseph Rwiza Kashushura, pamoja na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Mbinga (Mbinga TC), Amina H. Seif, wametembelea Banda la Mkoa wa Ruvuma katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), Julai 7, 2026.

Katika maonesho hayo, wajasiriamali kutoka Mkoa wa Ruvuma ni miongoni mwa washiriki waliopata nafasi ya kuonesha bidhaa na huduma zao, hatua inayowapa fursa muhimu ya kutangaza biashara zao, kupata masoko ya uhakika, kuunganisha mitandao ya kibiashara na kujifunza mbinu mbalimbali kutoka kwa wajasiriamali wengine wanaoshiriki maonesho hayo.

Maonesho ya 50 ya Sabasaba yanaendelea kuwa jukwaa muhimu la kukuza biashara, uwekezaji na ubunifu kwa kuwaunganisha wazalishaji, wajasiriamali, wawekezaji na wadau mbalimbali wa maendeleo ya uchumi kutoka ndani na nje ya Tanzania.









Na.Ashura Mohamed -Arusha


‎‎Wadau wa sekta ya kilimo, biashara, mazingira na teknolojia kutoka ndani na nje ya Afrika wanatarajiwa kukutana jijini Arusha katika Mkutano wa Kwanza wa Uchavushaji Afrika, unaolenga kuweka mkakati wa pamoja wa kulinda wachavushaji na kuimarisha kilimo endelevu barani Afrika.

‎Mkutano huo unatarajiwa kufanyika kuanzia Septemba 29 hadi Oktoba 1, 2026, ukiandaliwa na Shirika la Maendeleo Endelevu ya Kilimo na Biashara za Kilimo Tanzania (SAADIT) kwa kushirikiana na taasisi mbalimbali, ikiwemo Green Rural Community and workers bees Africa huku ukipata utambuzi rasmi kutoka Wizara ya Viwanda na Biashara.

‎Kupitia mkutano huo, wadau watajadili changamoto na fursa zinazohusu uchavushaji, pamoja na namna ya kuingiza uhifadhi wa wachavushaji katika sera na mipango ya maendeleo ili kuongeza uzalishaji wa mazao, kuimarisha usalama wa chakula na kukuza uchumi wa kilimo.

‎Mkurugenzi na Mwanzilishi wa SAADIT, Malulu Martin Igobeko, amesema kupungua kwa idadi ya wachavushaji kutokana na uharibifu wa mazingira na matumizi yasiyo sahihi ya viuatilifu ni tishio kwa mifumo ya uzalishaji wa chakula barani Afrika.

‎Amesema mkutano huo utakuwa jukwaa la kuunganisha serikali, sekta binafsi na washirika wa maendeleo katika kutafuta suluhisho la changamoto hiyo na kuhakikisha huduma za uchavushaji zinalindwa kwa maendeleo ya kilimo.

‎“Wachavushaji wanapungua kwa kasi kutokana na uharibifu wa maeneo wanayoishi na matumizi yasiyo sahihi ya viuatilifu. Bila wao, uzalishaji wa mazao na usalama wa chakula unaweza kuathirika,” amesema Igobeko.

‎Kwa upande wake, Genya Charles kutoka Wizara ya Viwanda na Biashara, amesema uchavushaji unapaswa kuonekana kama sehemu muhimu ya uchumi wa kijani na biashara, kutokana na mchango wake katika kuongeza thamani ya mazao na kufungua fursa za uwekezaji.

‎Naye Mercy Butta kutoka Idara ya Usalama wa Chakula katika Wizara ya Kilimo, amesema mchango wa nyuki na wachavushaji wengine ni muhimu katika kuongeza uzalishaji wa mazao na kuimarisha upatikanaji wa chakula nchini.

‎Katika mkutano huo, kampuni ya teknolojia ya ufugaji nyuki kutoka Australia, BeeSTAR Technology, inatarajiwa kuonyesha teknolojia za kisasa ikiwemo mizinga janja, matumizi ya akili bandia na mifumo ya kidijitali ya kufuatilia uzalishaji wa nyuki.

‎Teknolojia hizo zinatarajiwa kusaidia kuongeza uzalishaji wa asali, kupunguza upotevu wa mizinga na kuboresha huduma za uchavushaji katika sekta ya kilimo.

‎Aidha, mkutano huo utaangazia mpango wa kuongeza mizinga milioni moja unaolenga kuimarisha huduma za uchavushaji katika maeneo ya kilimo kupitia ushirikiano wa wadau mbalimbali.

‎Washiriki wa mkutano huo wakiwemo Green Rural Community and workers bees Africa, Innovative Community Solutions ( ICS), wanatarajiwa kujadili masuala ya utafiti, teknolojia, sera, uwekezaji na mikakati ya maendeleo kwa kushirikisha taasisi mbalimbali za kitaifa na kimataifa.






WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amesema kuna haja ya kutafuta mbinu mpya ya kukieneza Kiswahili baada ya kuwa kimepata hadhi ya kimataifa.

“Kadiri Kiswahili kinavyoendelea kupata hadhi ya kimataifa, ni muhimu sasa kuanza kutazama hatua inayofuata ya kukieneza duniani. Mataifa mengi yamefanikiwa kueneza lugha na utamaduni wao kupitia vituo vya utamaduni vilivyoanzishwa katika nchi mbalimbali duniani,” amesema.

Ametoa wito huo leo (Jumanne, Julai 7, 2026) wakati akizungumza na washiriki waliohudhuria kilele cha Maadhimisho ya Tano ya Siku ya Kiswahili Duniani kwenye ukumbi wa mikutano wa ofisi za makao makuu ya UNESCO jijini Paris, Ufaransa.

“Serikali itaendelea kuimarisha matumizi ya Kiswahili ndani na nje ya nchi kupitia elimu, tafiti, uchapishaji, tafsiri, teknolojia za kidijiti na diplomasia ya lugha. Tutaendelea kushirikiana na UNESCO, nchi mbalimbali, vyuo vikuu, taasisi za kimataifa na wadau mbalimbali katika kuendeleza lugha hii kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho,” amesema.

Waziri Mkuu ambaye alikuwa mgeni rasmi kwa niaba ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema sasa hivi Kiswahili kimeshatambulika kuwa lugha rasmi ya EAC na SADC. “Kiswahili ndiyo utambulisho wetu wana jumuiya ya Afrika Mashariki. Mtu akiongea Kiswahili anajulikana kuwa anatokea Tanzania, Burundi, Congo au Sudan Kusini. Na pia kimekuwa moja ya lugha rasmi za Umoja wa Afrika (AU),” amesema.

“Si hivyo tu, sasa hivi Kiswahili kinatambulika kuwa ni lugha rasmi ya mikutano mikubwa ya UNESCO kutokana na pendekezo lililopitishwa kwa kaulimoja Novemba, 2025 wakati wa Mkutano Mkuu wa 43 wa UNESCO, uliofanyika Samarkand, Uzbekistan.”

Amesema kwa mujibu wa wataalamu wa lugha, Kiswahili kinazungumzwa na watu kati ya milioni 300 hadi milioni 500 na idadi hiyo inaendelea kuongezeka kutokana na matumizi yake katika elimu, biashara, vyombo vya habari, teknolojia ya habari na mawasiliano pamoja na mitandao ya kijamii.

“Hali hiyo inaonesha kwamba Kiswahili siyo mali ya Watanzania pekee bali ni urithi wa Afrika na zawadi ya Afrika na dunia. Kiswahili kinaunganisha watu, Kiswahili kinaunganisha biashara, Kiswahili kinaunganisha jamii,” amesisitiza.

Mapema, Mkurugenzi Mkuu wa UNESCO, Prof. Khaled El-Enany aliwaeleza washiriki wa maadhimisho hayo kwamba shirika lake limesaidia kufadhili uandaaji wa kamusi ya Kifaransa kwenda Kiswahili.

“Mbali na matumizi ya kawaida kwa watalii au watu wanaojifunza lugha, tunatarajia kwamba uwepo wa kamusi hiyo na nyaraka nyingine kutasaidia kuongeza fursa kwa walimu na wanafunzi wanaojifunza Kifaransa na Kiswahili,” amesema.

Amesema uzuri wa Kiswahili ni lugha ambayo imekuwa ikiendelea kukua na kuvuka mipaka bila kupoteza uasili wake na imeunganisha watu bila kulazimika kuvuka mipaka ya nchi zao.

Akimkaribisha Waziri Mkuu kuzungumza na washiriki hao, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda alisema Tanzania ina lugha za makabila zaidi ya 150 katika maeneo mbalimbali lakini wananchi wake wameweza kuunganishwa na lugha moja ya Kiswahili.

Alisema wakati jijini Paris, Ufaransa wakiadhimisha kilele cha maadhimisho hayo na kongamano la pili lililoandaliwa na UNESCO kwa kushirikiana na Serikali ya Tanzania, nchi nyingine tatu za Uingereza, Algeria na Burundi nazo pia leo zimeadhimisha makongamano kama hayo.

Awali, Balozi wa Tanzania nchini Ufaransa, Bw. Saidi Othman Yakub alisema maadhimisho hayo ya tano ambayo yanafanyika sambamba na Kongamano la Pili la Siku ya Kiswahili Duniani, yamevutia washiriki zaidi ya 300 kutoka nchi 16 duniani.

Amezitaja nchi hizo kuwa ni Comoro, Tanzania, Ujerumani, Marekani, Canada, Uingereza, Italia, Luxembourg, Sweden, Ubelgiji, Austria, Uturuki, Misri, Kenya, Uganda na wengi kutoka Tanzania.

“Tangu tarehe 4 Julai hadi leo tarehe 7 Julai, 2026 tumeshuhudia shughuli mbalimbali zilizolenga kuendeleza na kukitangaza Kiswahili duniani. Shughuli hizo zilijumuisha matembezi ya hamasa katika mitaa maarufu ya Jiji la Paris, hafla za vyakula vya Kiswahili kwa Diaspora, kongamano kuhusu nafasi ya Kiswahili katika biashara na uchumi, semina na warsha mbalimbali hapa UNESCO.

Amesema waliandaa pia tamasha la Usiku wa Mswahili lililofanyika chini ya Mnara wa Eiffel kandokando ya Mto Seine, maonesho ya filamu na chakula pamoja na kazi za Kiswahili.

































 

Afisa Tawala wa Wilaya ya Morogoro, Bi. Janeth Chatta,akizungumza wakati akifunga mafunzo ya wasimamizi wa shughuli za ghala kwa msimu wa biashara wa mbaazi na dengu 2026/2027 yaliyofanyika wilayani humo kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya ya Morogoro.

Kaimu Mkurugenzi wa Uratibu na Ubora wa WRRB, Bw. Mwita Thomas,akizungumza wakati wa ufungaji mafunzo ya wasimamizi wa shughuli za ghala kwa msimu wa biashara wa mbaazi na dengu 2026/2027 yaliyofanyika Morogoro.

Sehemu ya washiriki wakimsikiliza Afisa Tawala wa Wilaya ya Morogoro, Bi. Janeth Chatta (hayupo pichani) wakati akifunga mafunzo ya wasimamizi wa shughuli za ghala kwa msimu wa biashara wa mbaazi na dengu 2026/2027 yaliyofanyika wilayani humo kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya ya Morogoro.

Afisa Tawala wa Wilaya ya Morogoro, Bi. Janeth Chatta akiwa katika picha ya pamoja na washiriki mara baada ya kufunga  mafunzo ya wasimamizi wa shughuli za ghala kwa msimu wa biashara wa mbaazi na dengu 2026/2027 yaliyofanyika wilayani humo kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya ya Morogoro.

Na.Mwandishi Wetu-MOROGORO

Watumishi na wasimamizi wa shughuli za ghala nchini wametakiwa kutekeleza majukumu yao kwa uadilifu, weledi na uwajibikaji ili kuimarisha Mfumo wa Stakabadhi za Ghala na kuongeza ufanisi katika biashara ya mazao ya kilimo.

Wito huo umetolewa na Afisa Tawala wa Wilaya ya Morogoro, Bi. Janeth Chatta, kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya ya Morogoro, alipokuwa akifunga mafunzo ya wasimamizi wa shughuli za ghala kwa msimu wa biashara wa mbaazi na dengu 2026/2027 yaliyofanyika wilayani humo.

Bi. Chatta amesema uadilifu wa watendaji wa mfumo ni msingi wa kujenga imani kwa wakulima, wanunuzi na taasisi za fedha, huku akisisitiza kuwa Mfumo huo umeendelea kuwa nyenzo muhimu ya kuhakikisha biashara ya mazao inafanyika kwa uwazi, ubora na ushindani.

Amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan inaendelea kuhimiza matumizi ya Mfumo huo pamoja na Soko la Bidhaa Tanzania (TMX) ili kuongeza thamani ya mazao, kupanua fursa za masoko yenye ushindani na kuongeza manufaa kwa wakulima.

Aidha, amewataka washiriki kutumia maarifa waliyoyapata kutekeleza majukumu yao kwa weledi, kuendana na mabadiliko ya teknolojia na kuhakikisha taarifa za mazao zinakuwa sahihi na kwa wakati.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Uratibu na Ubora wa WRRB, Bw. Mwita Thomas, amewataka wahitimu wa mafunzo hayo kuzingatia sheria, kanuni na taratibu walizofundishwa ili kutekeleza majukumu yao kwa uadilifu, weledi na uwajibikaji, pamoja na kulinda hadhi ya Mfumo wa Stakabadhi za Ghala.

Mafunzo hayo yaliyoandaliwa na WRRB yamefanyika kwa siku tano na yamehudhuriwa na washiriki 103 kutoka kampuni za uendeshaji wa ghala na wadau mbalimbali wa Mfumo huo.

 

Wafugaji nchini wanatarajiwa kunufaika na biashara ya kisasa ya mifugo baada ya Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) kuanza kuingiza mifugo katika Mfumo wa Stakabadhi za Ghala, utakaounganisha taarifa za mifugo kidijitali na kuwawezesha wanunuzi kushindana kwa uwazi kupitia Soko la Bidhaa Tanzania (TMX).

Akizungumza katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), Mkurugenzi Mtendaji wa WRRB, Bw. Asangye Bangu, amesema baada ya mafanikio ya kusimamia bidhaa 18 za mazao ya kilimo kupitia mfumo huo, sasa bodi imepanua huduma zake kwa kujumuisha mifugo.

Amesema hatua hiyo inatokana na mahitaji ya wafugaji waliokuwa wakihoji kwa nini mfumo huo unawanufaisha wakulima pekee huku sekta ya mifugo ikibaki nje.

"Tumekuja na bidhaa mpya ambazo zimeongezwa kwenye mfumo, na kubwa zaidi tumewafikia wafugaji. Tulikuwa tunasimamia bidhaa 18 za mazao ya kilimo, lakini sasa tumeingia rasmi kwenye bidhaa za mifugo," amesema.

Bw. Bangu amesema WRRB inalenga kuunganisha biashara ya mifugo na TMX, ambapo taarifa za kila mnyama zitawekwa kidijitali ili wanunuzi waweze kuzifikia kwa urahisi, kushindana kwa uwazi na kufanya maamuzi ya ununuzi kwa kutumia taarifa sahihi badala ya makadirio.

Ameeleza kuwa mfumo huo utatumia taarifa zinazopatikana kupitia hereni za utambuzi wa mifugo zilizozinduliwa na Rais Samia Suluhu Hassan, ambazo zina namba maalumu zinazobeba taarifa za kila mnyama.

"Tunafahamu Mheshimiwa Rais Samia miaka miwili iliyopita alizindua uwekaji wa hereni kwenye mifugo. Sisi kama WRRB tunapiga hatua zaidi kwa kutumia taarifa zilizopo kwenye hereni hizo kuingiza mifugo kwenye Mfumo wa Stakabadhi za Ghala. Hereni hiyo ndiyo itakuwa msingi wa stakabadhi kwa kuwa ina namba na taarifa zote za mnyama," amesema.

Amefafanua kuwa mfumo huo utawanufaisha wafugaji wanaojishughulisha na unenepeshaji wa mifugo kwa kuwa mifugo yao itahifadhiwa katika maeneo maalumu yatakayokuwa yanatambulika kama ghala, huku wafugaji wakipewa stakabadhi zitakazowawezesha kupata mikopo kutoka taasisi za fedha.

Kwa mujibu wa Bangu, WRRB tayari imefikia makubaliano na Benki ya NBC ambayo imekubali kutoa mikopo kwa wafugaji watakaoweka mifugo yao kwenye ghala.

"Wengi wanauliza ghala litakuwaje. Kwa upande wa mifugo, zizi ndilo litakuwa ghala. Mifugo itatunzwa katika maeneo maalumu yenye chakula na huduma za matibabu, huku mfugaji akiwa na stakabadhi inayomwezesha kupata fedha bila kulazimika kuuza mifugo yake mapema," amesema.

Bangu amesema hatua nyingine muhimu ni kuondoa utaratibu wa kupanga bei kwa kutazama mwonekano wa mnyama pekee, badala yake mifugo itapimwa kwa uzito ili bei iweze kuamuliwa kwa kuzingatia kilo halisi za mnyama.

"Leo hii kwenye minada mingi ng'ombe anapimwa kwa macho, anaonekana mnene au mwembamba ndipo bei inawekwa. Sisi tunataka mifugo ipimwe kwa uzito ili bei iwe ya haki kwa mfugaji na mnunuzi. Hii itakuwa mkombozi mkubwa kwa wafugaji na pia itarahisisha upatikanaji wa taarifa zinazohitajika katika masoko ya ndani na kimataifa," amesema.

 

Serikali imewaagiza wazalishaji wote nchini kutumia alama ya 'Made in Tanzania' ili kuongeza imani kwa bidhaa zinazozalishwa nchini na kuimarisha ushindani wake katika masoko ya kimataifa.

Agizo hilo limetolewa  na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Immanuel Nchimbi, kwenye kilele cha Usiku wa Jubilei ya Dhahabu (Miaka 50) ya Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TANTRADE), uliofanyika Ukumbi wa Mlimani City, Dar es Salaam. Sherehe hizo zilienda sambamba na utoaji wa tuzo kwa washirika muhimu wa mamlaka hiyo. Udhibiti wa Viwango na Huduma za Kifedha.

Aidha, Makamu wa Rais amezitaka taasisi zinazosimamia viwango na huduma za kifedha kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi ili kuhakikisha bidhaa za Tanzania zinakidhi viwango vya kimataifa. Alisema matumizi ya alama ya 'Made in Tanzania' yataongeza utambulisho wa bidhaa zenye ubora na kuimarisha heshima ya taifa katika biashara za kimataifa.

 "Nazipongeza taasisi za fedha kwa kutoa mikopo yenye masharti nafuu kwa viwanda vidogo na vya kati, akisema hatua hiyo imeendelea kupunguza changamoto za upatikanaji wa mitaji kwa wajasiriamali na kuchochea ukuaji wa uzalishaji nchini."amesema Balozi Nchimbi

Amesema Serikali itaendelea kuweka sera rafiki, kuboresha miundombinu na kuimarisha sekta binafsi ili kujenga uchumi wa viwanda wenye ushindani. Ameongeza kuwa maadhimisho ya Jubilei ya Dhahabu ya TANTRADE ni fursa ya kutathmini mafanikio yaliyopatikana, ikiwemo kuongezeka kwa viwanda, uzalishaji, ajira na upanuzi wa masoko ya bidhaa za Tanzania duniani.

Kwa upande wake Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Judith Kapinga (Mb), amesisitiza kuwa manufaa makubwa ya rasilimali zilizopo nchini yatapatikana Tanzania itakapowekeza katika kuchakata na kuzalisha bidhaa za mwisho zenye ubora wa juu badala ya kuuza malighafi ghafi nje ya nchi.

Waziri Kapinga amebainisha kuwa hatua hiyo itafungua masoko mapya, itaongeza thamani ya mauzo ya nje, na kuinua uchumi wa wananchi kwa ujumla.

Mhe. Kapinga ameeleza kuwa, ili kujenga uchumi imara wa viwanda na wenye ushindani, kuna haja ya kubadili mtazamo wa kibiashara kwa kuhakikisha mazao ya kilimo, mifugo, uvuvi, misitu na madini yanageuzwa kuwa bidhaa zilizofungashwa vizuri na kukidhi viwango vya kimataifa.

Amesisitiza kuwa uwekezaji mkubwa katika teknolojia za kisasa una mchango mkubwa katika kuongeza kiwango cha uzalishaji, kuboresha ubora wa bidhaa zinazotengenezwa nchini, kupunguza gharama za uendeshaji, na kuzipa bidhaa za Tanzania uwezo mkubwa wa kushindana katika soko la kimataifa.


Top News