Taasisi ya Jumuiya ya Tabia za Kiislam (JAI ) imepanga kuwalisha wagonjwa zaidi ya 1,800 katika hospitali mbalimbali wakati wa sikukuu ya Eid al‑Fitr, ikiwa ni sehemu ya kuwafariji na kuwafanya wajione kuwa ni sehemu ya jamii licha ya changamoto za kiafya wanazopitia.

Akizungumza katika hafla ya uchangiaji iliyoandaliwa kwa ajili ya kufanikisha zoezi hilo, Katibu wa JAI, Ramadhani Kombo, amesema jumuiya hiyo imejipanga kuhakikisha wagonjwa wanasherehekea sikukuu hiyo kwa furaha kama Watanzania wengine.

Amesema matarajio yao ni kuwafikia wagonjwa zaidi ya 1,800 kwa kuwapatia chakula maalum cha sikukuu, huku makadirio ya bajeti ya kufanikisha zoezi hilo yakifikia shilingi milioni 22.

“Tumekutana hapa kuhamasisha wadau na watu wenye mapenzi mema kujitokeza kuchangia kwa hali na mali ili kufanikisha zoezi hili. Lengo letu ni kusherehekea sikukuu pamoja na wagonjwa ili nao wajione ni sehemu ya Watanzania, kwani maradhi ni mitihani ya maisha,” amesema Kombo.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa JAI, Ridhiwani Mpanju amesema taasisi hiyo ilianzishwa mwaka 2008 kabla ya kusajiliwa rasmi mwaka 2014, ikiwa na dhamira ya kuwahudumia wagonjwa na kuwapa faraja katika kipindi wanachopitia changamoto za kiafya.

Amesema kupitia makao makuu ya jumuiya hiyo yaliyopo Magomeni, wamekuwa wakitekeleza shughuli mbalimbali za kijamii ikiwemo kuwapatia wagonjwa uji wa asubuhi na chakula cha kufuturu wakati wa mwezi wa Ramadhani, pamoja na kusaidia kulipia bili za wagonjwa waliokwama hospitalini.

Ameongeza kuwa katika kusherehekea Eid al‑Fitr mwaka huu, jumuiya hiyo imepanga kuandaa chakula maalum na kula pamoja na wagonjwa hao ili kuwapa faraja na kuwafanya wajisikie kuthaminiwa na jamii.

Kutokana na mpango huo, viongozi wa jumuiya hiyo wamewaomba waumini wa dini ya Kiislamu pamoja na wadau wengine wa maendeleo kujitokeza kuchangia ili kufanikisha lengo la kuwafikia wagonjwa hao zaidi ya 1,800 siku ya sikukuu.






Shirika la Viwango Tanzania (TBS) limetoa mafunzo kwa wajasiriamali wanaozalisha nishati safi ya kupikia, hususan mkaa mbadala, mkoani Kigoma kwa lengo la kuwajengea uwezo wa kuzalisha bidhaa zinazokidhi matakwa ya viwango.

Mafunzo hayo yamelenga kuwasaidia wazalishaji hao kuboresha ubora wa mkaa mbadala wanaozalisha ili uweze kukidhi mahitaji ya soko la ndani na nje ya Tanzania.

Akizungumza wakati wa mafunzo hayo, Afisa Viwango wa TBS, Bw. Spiradson Kagaba, amesema matumizi ya mkaa mbadala yana faida nyingi ikiwemo kupunguza taka, kutotoa moshi unaodhuru afya, kuwaka kwa muda mrefu na kusaidia kulinda uoto wa asili kwa kupunguza ukataji wa miti.

Amesema kuwa matumizi ya nishati hiyo ni hatua muhimu katika kulinda mazingira na kuboresha afya za watumiaji wa nishati za kupikia.

Aidha, wazalishaji hao wametakiwa kuzingatia viwango vilivyowekwa ili kuhakikisha wanazalisha bidhaa zenye ubora unaotakiwa, kulinda afya za watumiaji na kuhifadhi mazingira.

“Hatua hii inaunga mkono mkakati wa Serikali wa kupunguza ukataji wa miti na kuhamasisha matumizi ya nishati rafiki kwa mazingira,” amesema Kagaba.



 

Na Mwandishi wetu- Dodoma

 Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu imeendelea na hatua ya tatu ya kujengewa uwezo  wa namna ya kufanya tathmini za programu na miradi kupitia programu ya Kuendeleza  Sekta ya Kilimo Awamu ya Pili (ASDP II)  ili kuwawezesha watalaam wa ufuatiliaji na tathmini kupata uelewa na namna ya kutathmini miradi na programu mbalimbali zinazotekelezwa katika taasisi za umma.


Hayo yamesemwa leo tarehe 16 Machi 2026, jijini Dodoma na Mkurugenzi wa Ufuatiliaji na Tathmini ya Utendaji wa Serikali, Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Bi. Sakina Mwinyimkuu   wakati akifungua mafunzo yanayofanyika kwa siku nne Jijini Dodoma yakihusisha washiriki kutoka wizara zinazotekeleza  program ya ASDP II na washiriki kutoka nchini Zimbabwe na Malawi kwa lengo la kujifunza chini ya Twendembele Initiative ambapo Tanzania ni mshirika.

 


Bi. Sakina amewasisitiza washiriki kuzingatia mafunzo kwani yatawasaidia katika kuimarisha eneo la tathmini kwa ujumla yanayotolewa na Watathmini wazawa wa Kampuni ya Auxim na Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine mkoani Morogoro huku yakiratibiwa  na Clear Initiatives kwa ufadhili kutoka Global Evaluation Initiative iliyopo chini ya Benki ya Dunia.

 “Mabadiliko ya sekta ya kilimo yanaendelea kuwa msingi wa mikakati ya maendeleo katika Afrika Mashariki na Kusini, ambapo mifumo ya kilimo cha wakulima wadogo ina jukumu muhimu katika kudumisha maisha ya vijijini, kuhakikisha usalama wa chakula, na kuchochea ukuaji wa uchumi wa kitaifa” amesema Mkurugenzi huyo.

 


Ameongeza kuwa, mpango wa Maendeleo ya Sekta ya Kilimo Awamu ya Pili (ASDP II) unasimama kama mpango wa ushirikiano wa wadau wengi, ukiwa na lengo la kuongeza uzalishaji wa kilimo, kukuza ujumuishaji wa masoko, kuendeleza uendelevu wa mazingira, na kuimarisha ushiriki jumuishi wa kiuchumi miongoni mwa wakulima wadogo na jamii za vijijini.

 


“Mnamo Desemba 2024, Ofisi ya Waziri Mkuu – Idara ya Sera, Mipango na Uratibu (PMO-PPCD) iliingia katika ushirikiano na kituo cha kujifunza kuhusu tathmini na matokeo – Afrika ya Anglophone (CLEAR-AA) cha Global Evaluation Initiative (GEI) katika Wits School of Governance pamoja na Taasisi ya Ujerumani ya Tathmini ya Maendeleo (DEval) ili kufanya tathmini ya matokeo ya ASDP II,” ameongeza.

 


Vilvile amefafanua kwamba, ushirikiano huo unaonyesha dhamira ya makusudi ya kuzingatia viwango vya kimataifa vya tathmini huku ukihakikisha kuwa mchakato wa tathmini unabaki katika umiliki wa kitaifa na unachangia kujifunza kwa taasisi.

 “Mfumo huu wa ushirikiano umeundwa kuunganisha umakini wa kitaalamu, uimara wa mbinu, na mbinu bora za kimataifa, huku ukihakikisha kuwa serikali zinazoshiriki zinabaki na umiliki kamili wa mchakato na matokeo yake,” alieleza Mkurugenzi huyo.

Pia ameeleza kwamba, warsha hiyo  inawaleta pamoja wawakilishi kutoka nchi mbalimbali. wakiwemo wadau wakuu wa kitaasisi  ambao ni pamoja na Serikali ya Tanzania, inayowakilishwa na PMO-PPCD na Wizara zinazoongoza Sekta ya Kilimo zinazohusika katika utekelezaji wa program,  Serikali ya Zimbabwe kupitia Ofisi ya Rais na Baraza la Mawaziri – Kurugenzi ya Tathmini, Kujifunza na Utafiti,  na Serikali ya Malawi, inayowakilishwa na Wizara ya Fedha, Mipango ya Uchumi na Ugatuzi.

“Mtandao wa kikanda wa tathmini wa Twende Mbele unashiriki pia, ukichangia utaalamu wa kulinganisha na kuwezesha ujifunzaji wa pamoja kati ya mifumo ya tathmini barani Afrika. Muundo huu wa utawala wa wadau wengi unaonyesha dhamira inayokua ya kikanda ya kuingiza utamaduni wa tathmini ndani ya mifumo ya kitaifa,” amesema.

Aidha, ameeleza kwamba  sifa mojawapo muhimu ya tathmini  inayoongozwa na Nchi (Country-Led Evaluation) ni ujumuishaji wa makusudi wa maendeleo ya uwezo wa kitaasisi kama sehemu kuu ya mchakato, badala ya kuwa shughuli ya ziada kwani maendeleo endelevu katika utawala unaotumia ushahidi hayategemei tu uzalishaji wa matokeo ya tathmini, bali pia kuimarisha uwezo wa taasisi kuagiza, kusimamia na kutumia tathmini kwa muda mrefu.


Na Mwandishi Wetu

LICHA ya wanawake kumiliki au kuendesha zaidi ya nusu ya biashara ndogo na za kati nchini, ushiriki wao katika nafasi za juu za maamuzi ndani ya taasisi za fedha bado uko chini ya asilimia 30, jambo linaloibua mjadala kuhusu usawa wa kijinsia katika sekta hiyo.

Hoja hiyo inatarajiwa kujadiliwa na wadau wa sekta ya fedha katika mkutano wa tatu wa Chama cha Wanawake katika Sekta ya Fedha Tanzania (TAWiFA) utakaofanyika Machi 23, 2026 mjini Arusha.

Akizungumza leo Machi 16, 2026 kuelekea mkutano huo, Rais wa  TAWiFA, Fikira Ntomola, amesema bado kuna changamoto zinazoathiri wanawake kupata fursa sawa katika sekta ya fedha, hasa katika nafasi za uongozi na upatikanaji wa huduma za kifedha.

“Pamoja na ongezeko la matumizi ya huduma za kifedha nchini, wanawake wengi bado wanakumbana na vikwazo vya kupata mikopo au mitaji kwa ajili ya kukuza biashara zao, hivi karibuni tutaanza utafiti kuangalia changamoto zinazowakabili wanawake kwenye msawala ya fedha ili waweze kuona namna ya kuwasaidia,” amesema.

Kwa mujibu wa utafiti wa FinScope Tanzania wa mwaka 2023, kiwango cha ujumuishaji wa kifedha nchini kimeongezeka kwa kiasi kikubwa katika kipindi cha zaidi ya muongo mmoja uliopita. 

Takwimu zinaonyesha asilimia 76 ya Watanzania wazima sasa wanatumia huduma za kifedha, ikilinganishwa na takribani asilimia 16 mwaka 2009.

Hata hivyo, wadau wa sekta hiyo wanasema bado kuna pengo kati ya wanaume na wanawake katika kunufaika na baadhi ya huduma za kifedha, hususan mikopo ya biashara na uwekezaji.

Takwimu za taasisi za maendeleo ya biashara ndogo na za kati zinaonyesha kuwa wanawake wanamiliki au kuendesha zaidi ya asilimia 50 ya biashara ndogo na za kati nchini, sekta inayochangia kwa kiasi kikubwa katika ajira na ukuaji wa uchumi.

Katika ukanda wa Afrika Mashariki, tafiti zinaonyesha kuwa biashara zinazoendeshwa na wanawake zinachangia takribani asilimia 40 ya shughuli za kiuchumi, hali inayodhihirisha mchango mkubwa wa wanawake katika maendeleo ya uchumi wa nchi.

“Hata hivyo, pamoja na mchango huo, ushiriki wa wanawake katika nafasi za juu za maamuzi ndani ya taasisi nyingi za kifedha bado ni mdogo,” amesema.

Utafiti uliofanywa na McKinsey & Company unaonyesha kuwa taasisi zenye uwiano mzuri wa kijinsia katika uongozi zina uwezekano mkubwa zaidi wa kufanya vizuri kiutendaji na kifedha kuliko zile zenye uwiano mdogo wa kijinsia.

Kwa upande wake, Meneja wa Habari na Mawasiliano kwa Umma wa Mamlaka ya Bima Tanzania (Tira), Hadija Maulidi, alisema mkutano huo unatarajiwa kuwa chachu ya kuongeza ushiriki wa wanawake katika sekta ya fedha.

“Kwa upande wa bima ambayo ni sehemu ya sekta ya fedha, ushiriki wa wanawake unaendelea kuongezeka. Katika mkutano huu pekee zaidi ya wanawake 40 kutoka mamlaka yetu wanatarajiwa kushiriki,” ameongeza.

Pia amesema kupitia mamlaka hiyo wataendelea kuhamasisha wanawake kushiriki kikamilifu katika soko la bima ili waweze kuchangia zaidi katika ukuaji wa sekta ya fedha na pia kushika nafasi za juu za uongozi.

Mbali na mkutano huo, waandaaji pia wanatarajia kutoa mafunzo ya elimu ya fedha kwa wanawake wajasiriamali 200 kabla ya mkutano huo. Baada ya mkutano, washiriki wanatarajiwa kushiriki zoezi la upandaji miti 2,000 katika shule 10 za msingi zilizochaguliwa mkoani Arusha.

Mkutano huo utawakutanisha wadau kutoka sekta za benki, bima, masoko ya mitaji, mifuko ya pensheni pamoja na mamlaka za udhibiti wa sekta ya fedha ili kujadili namna ya kuimarisha ujumuishaji wa kifedha na kuongeza ushiriki wa wanawake katika uongozi wa sekta hiyo.



Mapinduzi ya nishati ya umeme katika Jimbo la Katoro yameingia hatua mpya leo, baada ya kupokelewa kwa gari maalum la Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) lenye uwezo wa kubeba tani saba (7), likilenga kurahisisha usambazaji wa huduma.

Gari hilo limekuja wakati muafaka ambapo TANESCO imeanza kutumia nguzo za zege ambazo ni imara zaidi lakini zina uzito mkubwa ukilinganishwa na nguzo za miti zilizokuwa zikibebwa na watu hapo awali.

Kaimu Meneja wa TANESCO Mkoa wa Geita, Mhandisi Michael Mbwana, amebainisha kuwa gari hilo ni ukombozi katika ubebaji wa nguzo hizo nzito na litaongeza ufanisi wa kazi maeneo ya vijijini na mjini.

Akizungumza na wananchi waliojitokeza kulipokea gari hilo, Mbunge wa Jimbo la Katoro, Mhandisi Kija Limbu Ntemi, ametoa habari njema kuwa vitongoji 64 vilivyosalia sasa vitafikiwa na umeme kwa kasi zaidi.

"Gari hili litaongeza kasi ya usambazaji wa umeme. Nawaomba wananchi tushirikiane ili kwa pamoja tuijenge Katoro Mpya yenye nishati ya uhakika," alisema Mhandisi Kija.

Kufuatia kukua kwa Mamlaka ya Mji Mdogo wa Katoro na ongezeko la mahitaji ya umeme, Shirika hilo limeipandisha hadhi Katoro na kuifanya kuwa Wilaya ya Ki-TANESCO. 

Hatua hii inalenga kusogeza huduma za kiufundi na kiutawala karibu zaidi na wananchi ili kumaliza kero za kukatika kwa umeme na ucheleweshaji wa maunganisho mapya.

 Mbunge wa Jimbo la Geita Vijijini, Mhe. Joseph Kasheku (Msukuma), aliyekuwepo eneo hilo, amesema kasi ya ukuaji wa Katoro inatosha kuifanya kuwa Halmashauri inayojitegemea.

Mhe. Msukuma amemshauri Mhandisi Kija kupambana kuhakikisha Katoro inapata hadhi ya Halmashauri ili kuwapunguzia wananchi adha ya kusafiri umbali mrefu kufuata huduma za kiserikali na kuchochea maendeleo ya mji huo wa kibiashara.

Nao wananchi wa Katoro wameonyesha kufurahishwa na hatua hiyo, wakisema kuwa kuwasili kwa vitendea kazi hivyo na kupanda hadhi kwa ofisi za TANESCO ni ishara ya wazi kuwa Katoro inakwenda kuwa kitovu kikubwa cha uchumi mkoani Geita.









Na Farida Mangube Dar es salaam

Wanawake na wasichana nchini wamehimizwa kutumia teknolojia na majukwaa ya kidijitali kwa njia sahihi ili kujijengea uwezo wa kiuchumi, kielimu na kijamii hatua itakayochangia kufikia malengo ya maendeleo ya taifa kuelekea Dira ya Maendeleo ya Tanzania ya mwaka 2050.

Wito huo umetolewa na Kaim Mkurugenzi mtendaji wa shirika la CAMFED Tanzania Bi. Ana Sawaki kwenye kikao kazi Cha siku moja kilichoandaliwa na CAMFED kwa kushindana na Plan international chenye lengo la kuwajengea uwezo wasichana na wanawake katika masuala ya uongozi, usawa wa kijinsia pamoja na matumizi sahihi ya teknolojia na akili bandia (AI).

Kikao hicho kimefanyika makao makuu ya CAMFED kimewaleta pamoja wasichana na wanawake kutoka maeneo mbalimbali kwa lengo la kuimarisha uelewa wao kuhusu matumizi salama na yenye tija ya mitandao ya kijamii na teknolojia za kisasa.

Akizungumza katika kikao hicho, Mkurugenzi huyo amesema kuwa mitandao ya kijamii na teknolojia za kidijitali zimefungua fursa kubwa za kujifunza, kufanya biashara na kupata taarifa muhimu, lakini pia zinaweza kuwa chanzo cha kupotoshwa au kuharibika kwa maadili endapo zitatumika vibaya.

Amesisitiza kuwa wasichana wanapaswa kujifunza na kutumia teknolojia kwa kuchagua maarifa sahihi yanayozingatia maadili na mwelekeo wa maendeleo ya Tanzania.

“Mitandao ina fursa kubwa ya kujifunza, lakini pia ina hatari ya kuharibika kama haitatumika vizuri. Hivyo ni muhimu kwa wasichana kujifunza mambo sahihi yanayoendana na maadili ya nchi yetu na malengo ya maendeleo ya taifa,” alisema.

Aidha, amewahimiza wasichana na wanawake kufanya kazi kwa bidii na kujihusisha na shughuli za maendeleo zenye staha ili kujijengea uwezo wa kujitegemea kiuchumi.

Kwa mujibu wake, mwanamke anapokuwa na uwezo wa kiuchumi hupata nafasi kubwa ya kushiriki katika kufanya maamuzi ndani ya familia na jamii kwa ujumla.

“Wanawake wanapokuwa na uwezo wa kiuchumi wanapata nguvu ya kufanya maamuzi katika jamii. Hivyo ni muhimu kuwekeza katika elimu, ujuzi na teknolojia ili kuongeza uwezo huo,” aliongeza.

Katika mafunzo hayo pia ilielezwa kuwa dhana ya uwezeshaji wa wanawake (Women Empowerment) haipaswi kutafsiriwa kama ushindani dhidi ya wanaume, bali ni mchakato wa kumwezesha mwanamke kujitambua, kujenga uwezo wake na kutumia vipaji alivyonavyo kuchangia maendeleo ya jamii.

Washiriki wa kikao hicho walipata mafunzo mbalimbali ikiwemo matumizi sahihi ya akili bandia (AI), usalama wa mtandaoni, pamoja na namna teknolojia inavyoweza kuwa nyenzo muhimu katika kujenga uongozi wa wanawake na kukuza usawa wa kijinsia.

Shirika la CAMFED ambalo limekuwa mstari wa mbele katika kuendeleza elimu ya wasichana barani Afrika, linaamini kuwa teknolojia ya kidijitali ni nyenzo muhimu katika kuwafikia wasichana wengi zaidi na kuwapa fursa za elimu, ajira na uongozi.

Navina Mutabazi ni mwezeshaji wanawake kidijitali anasema matumizi sahihi ya teknolojia kwa wasichana wanaweza kupata maarifa mapya, kuanzisha biashara za kidijitali, kujifunza stadi za kisasa pamoja na kushiriki katika mijadala ya maendeleo inayohusu taifa.

Hatua hivyo inaendana na mwelekeo wa maendeleo ya taifa unaolenga kujenga jamii yenye usawa wa kijinsia, ubunifu na matumizi makubwa ya teknolojia kuelekea Tanzania yenye uchumi wa kisasa ifikapo mwaka 2050.

Kupitia programu zake za uongozi na uwezeshaji wa wasichana, CAMFED inaendelea kuwajengea uwezo wasichana na wanawake ili wawe viongozi wa sasa na baadaye, huku wakitumia teknolojia kama nyenzo ya kuharakisha maendeleo yao binafsi na ya jamii kwa ujumla.

Mafunzo hayo pia yamewapa washiriki nafasi ya kujifunza namna ya kutumia teknolojia kwa uwajibikaji, kuzingatia maadili ya jamii na kuhakikisha kuwa maarifa wanayopata mtandaoni yanachangia maendeleo ya taifa.



NA EMMANUEL MBATILO, MICHUZI TV

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Elimu, Utamaduni na Michezo imeridhishwa na kukamilika kwa jengo jipya la TEHAMA katika Chuo cha Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (CoICT) cha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), ikisema mradi huo ni hatua muhimu katika kuimarisha uwezo wa Tanzania katika teknolojia zinazoibukia.

Kamati hiyo iliyoongozwa na Mwenyekiti wake, Husna Sekiboko, ilitembelea leo Machi 16, 2026 kituo hicho kwa lengo la kukagua maendeleo ya mradi huo na kuthibitisha kuwa ujenzi wa jengo hilo umekamilika. Vifaa muhimu kwa ajili ya kituo hicho tayari vimewasili na vinasubiri kufungwa kabla ya kuanza kwa shughuli za ufundishaji na utafiti.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Sekiboko amesema Akili Unde ni moja ya mapinduzi makubwa ya kiteknolojia katika dunia ya sasa, hivyo Tanzania inapaswa kujipanga kutumia fursa zinazotokana na teknolojia hiyo huku ikikabiliana na changamoto zake.

“Mapinduzi ya teknolojia katika kompyuta ni makubwa sana na yataendelea kwa miaka mingi. Baadhi ya kazi zinazofanywa na binadamu kwa sasa zinaweza baadaye kufanywa na kompyuta,” amesema.

Ameongeza kuwa miradi inayotekelezwa na vyuo vikuu mbalimbali nchini inaonesha matumizi mazuri ya fedha za umma na ina uwezo mkubwa wa kuchangia ukuaji wa uchumi wa taifa.

“Miradi tuliyoitembelea inaonesha wazi kuwa rasilimali za umma zinatumika kwa ufanisi na zinaweza kuleta manufaa makubwa kwa uchumi wa nchi,” amesema.

Kwa upande wake, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda, amesema serikali imejipanga kuongeza wataalamu katika eneo la Teknolojia ya Habari na Mawasiliano pamoja na Akili Unde kwa kusomesha Watanzania nje ya nchi, sambamba na kuimarisha miundombinu na vifaa vya kisasa vya kufundishia na kujifunzia.

Amesema kupitia mpango wa Samia Scholarship, serikali tayari imepeleka wanafunzi katika vyuo vikuu mahiri nchini Afrika Kusini na Ireland kusoma masomo ya Akili Unde, Sayansi ya Data na Sayansi Shirikishi.

“Pamoja na kupeleka wanafunzi kusoma nje ya nchi, tuna chuo cha Indian Institute of Technology Zanzibar ambapo tunapeleka wanafunzi wa eneo hilo katika ngazi ya uzamili,” amesema Prof. Mkenda.

Aidha, amewataka vijana kuona fursa kubwa zinazokuja kupitia maendeleo ya teknolojia, ambazo zinaweza kufungua milango ya ajira na ubunifu, huku akisisitiza matumizi sahihi na salama ya teknolojia hizo.

Akizungumzia ujenzi wa miundombinu unaofanywa na serikali katika ndaki hiyo, amesema utakapokamilika utaongeza udahili wa wanafunzi wapatao 351, huku pia ukiwa umechangia kutoa ajira 529 zikiwemo za kitaaluma na za muda mfupi.

Naye Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Prof. William Anangisye, amesema kituo hicho kipya cha AI kitaiweka UDSM katika nafasi ya kuwa kitovu muhimu cha mafunzo na utafiti wa teknolojia za kisasa katika ukanda huu.

Amesema jengo hilo litasaidia kuendeleza utafiti wa kisasa katika Akili Unde, Sayansi ya Data na ubunifu wa kidijitali, pamoja na kuimarisha ushirikiano kati ya chuo kikuu, sekta ya viwanda na taasisi za kimataifa za utafiti.



























Top News