Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Uganda Mhe. Yoweri Kaguta Museveni mara baada ya kuwasili katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 07 Februari, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Uganda Mhe. Yoweri Kaguta Museveni akisaini Kitabu cha wageni mara baada ya kuwasili katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 07 Februari, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha ya pamoja na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Uganda Mhe. Yoweri Kaguta Museveni mara baada ya kuwasili katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 07 Februari, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Uganda Mhe. Yoweri Kaguta Museveni mara baada ya kuwasili katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 07 Februari, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiongoza ujumbe wa Tanzania kwenye mazungumzo ya pamoja na Ujumbe wa Uganda uliongozwa na Rais wa Jamhuri ya Uganda Mhe. Yoweri Kaguta Museveni katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 07 Februari, 2026. 
 


*📌 Wateja wa awali zaidi ya elfu 20 kuunganishwa na huduma ya umeme katika Vitongoji vya mkoa huo. *

Morogoro📍


Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Mhe. Adam Malima, tarehe 6 Februari, 2026 amewapokea wakandarasi wawili kutoka Wakala wa Nishati Vijijini (REA); watakaotekeleza Mradi mkubwa wa kusambaza umeme katika vitongoji 570 vya mkoa huo; ikielezwa kuwa Mradi huo una thamani ya shilingi bilioni 91.

Wakandarasi hao ni kampuni ya Sagemcom Energy & Telecom SAS (Italia) na China Railway No. 4 Engineering Group Co. Ltd (China) ambao watasambaza umeme katika vitongoji 570 katika Mradi huo mkubwa kwa gharama ya shilingi bilioni 91.

Akizungumza wakati wa hafla ya kuwatambulisha wakandarasi hao, Mhe. Malima alisema Mradi huo ni utekelezaji wa dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita ya kuhakikisha Watanzania wote wanapata huduma ya umeme wa uhakika hususan maeneo ya vijijini.

Mhe. Malima alisema kuwa Serikali kupitia REA imeleta maendeleo makubwa kwenye Sekta ya Nishati hususan kwenye usambazaji wa umeme vijijini katika kipindi cha miaka 15; akitolea mfano wakati alipokuwa Naibu Waziri wa Nishati mwaka 2008 ambapo bajeti ya REA ilikuwa shilingi bilioni tano pekee.

“Leo hii baada ya miaka 15 mkoa wa Morogoro pekee yake, unatekeleza Miradi ya umeme yenye thamani ya shilingi bilioni 91. Hii inaonesha dhamira ya dhati ya Serikali katika kuhakikisha Wananchi wa vijijini wanapata umeme kwa maendeleo yao ya kiuchumi na kijamii.” alisema Mhe. Malima.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Umeme Vijijini, Mhandisi, Thomas Mmbaga kutoka REA alisema wamewatambulisha rasmi wakandarasi wawili watakaofanya kazi ya kusambaza umeme kwenye vitongoji 570 kwa mgawo wa kampuni ya Sagemcom Energy ambayo itasambaza umeme katika vitongoji 325 na kuunganisha wateja wa awali 11,399 katika wilaya ya Mvomero; Morogoro Vijijini na Gairo kwa gharama ya shilingi bilioni 48.4.

Mkandarasi wa pili ni kampuni ya China Railway No. 4 ambayo itasambaza umeme kwenye vitongoji 245 na kuunganisha wateja wa awali 8,649 katika wilaya ya Kilosa; Malinyi; Kilombero na Ulanga kwa gharama ya shilingi bilioni 42.5 ambapo kipindi cha utekelezaji kwa Mradi huo katika mkoa wa Morogoro ni miaka mitatu.

Naye Meneja wa TANESCO mkoa wa Morogoro, Mhandisi, Zawadi Macha alisema Shirika hilo limejipanga kikamilifu kusimamia utekelezaji wa Mradi huo kwa karibu ili kuhakikisha unatekelezwa kwa ubora unaotakiwa na kwa kuzingatia viwango vilivyowekwa.

Kwa upande wake, Meneja wa Mradi wa Kampuni ya Sagemcom Energy, Bwana Calvin Manase alisema kampuni hiyo ina uzoefu mkubwa katika utekelezaji wa miradi ya umeme na imejipanga kuhakikisha mradi unakamilika ndani ya miezi 34 licha mkataba kuwa miezi 36.

Manase aliongeza kuwa kampuni hiyo itatoa ajira kwa Wananchi (Wazawa) wa maeneo husika ili wanufaike moja kwa moja wakati wa utekelezaji wa Mradi huo. Aidha, ameipongeza REA kwa mpango wake wa kulipa malipo ya awali kwa wakandarasi akisema hatua hiyo itasaidia kupunguza changamoto ya upatikanaji wa vifaa vya ujenzi wa Mradi huo.







Kaimu Mkurugenzi Idara ya Ushirikiano wa Kiufundi kwa Afrika Gashaw Gebeyehu Wolde wa Shirika la Kimataifa la Nguvu za Atomiki (IAEA)akizungumza na waandishi  wa habari mara baada ya kutembembelea mashine za kisasa katika Taasisi ya Ocean Road jijini Dar es Salaam.
Mtendaji  Mkuu wa Taasisi ya Ocean Road Dkt.Diwani Msemo akizungumza kuhusiana na mikakati ya Taasisi mara baada ya kutembelewa na IAEA jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mkuu wa Nguvu za Atomu Tanzania (TAEC) Profesa Najat Kassim Mohammed akizungumza kuhusiana na ujio wa IAEA katika Taasisi ya Ocean Road kuangalia mashine za miozi, jijini Dar es Salaam.


*Waahidi kuwa wa kwanza kudhibitisha Ithibati ya ubora.

Na Mwandishi Wetu
SHIRIKA la Kimataifa la Nguvu za Atomiki (IAEA) limesema kuwa Taasisi ya Ocean Road imefanya mageuzi katika utoaji huduma za saratani.

Akizungumza katika ziara ya Shirika hilo likiongozwa na Kaimu Mkurugenzi Idara ya Ushirikiano wa Kiufundi kwa Afrika Gashaw Gebeyehu Wolde amesema Taasisi ya Ocean Road katika imefanya mageuzi makubwa ya kuwa na vifaa vya teknolojia katika otoaji wa huduma za Saratani ikilinganishwa na miaka iliyopita wakati walipotembelea.

Wolde amesema katika hatua ambayo imefikiwa watakuwa watu kwanza katika kupitisha ithibati ya ubora ya huduma ya Saratani na kufanya Taasisi ya Ocean Road kuwa ya Tatu Afrika katika utoaji huduma hiyo.

Amesema Serikali ya Tanzania imewekeza katika kuwa na miundombinu pamoja na vifaa vya Kisasa ikiwemo za ugunduzi wa saratani za aina mbalimbali.

Aidha amesema IAEA itaendelea kutoa ushirikiano kwa Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI) ili kuimarisha ushirikiano, ikiwa ni pamoja na mafunzo ya matumizi ya mashine za CT-Scan na kutoa vifaa vya mionzi na kusomesha wataalam katika ubobezi wa magonjwa ya saratani.

Hata hivyo Wolde ametoa shukurani kwa Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa ununuaji wa mashine za kisasa na fedha nyingi katika Taasisi ya Ocean Road.

Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Ocean Road Dkt.Diwani Msemo amesema kuwa ujumbe IAEA wametembelea mashine mbalimbali na kuona Taasisi hiyo imejipanga.

Amesema miundombinu na vifaa tiba vilivyopo vimeongeza huduma katika kutoa huduma kwa mgonjwa bila kuathiri .

Hata hivyo amesema ujumbe huo umekiri kuwa mashine zilizopo za kisasa katika hospitali za Afrika Mashariki.

Mkurugenzi Mkuu wa Nguvu za Atomu Tanzania (TAEC) Profesa Najat Kassim Mohammed amesema Taasisi ya Ocean Road imepiga hatua kubwa katika utoaji wa huduma ya Saratani.

Aidha ametoa shukurani kwa Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan katika uwezeshaji wa vifaa vya kisasa katika Taasisi ya Ocean kwa kutumia Fedha za ndani.



Baadhi ya matukio katika ziara ya IAEA kwenye Taasisi ya Ocean Road Jijini Dar es Salaam
Na. OWM - KAM (DSM)

Mamia ya Vijana kutoka Mikoa mbalimbali nchini wamejitokeza katika Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) kushiriki zoezi la usajili wa madereva wanaotarajia kwenda kufanya kazi nchini Qatar.

Zoezi hili ni sehemu ya utekelezaji wa programu ya Serikali ya kuwaunganisha Watanzania na fursa za Ajira nje ya nchi kupitia mifumo rasmi ili kuhakikisha ulinzi wa haki na usalama wao.

Kaimu Mkurugenzi wa Huduma za Ajira, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano Jane Sorogo, amebainisha kuwa mwitikio umekuwa mkubwa ambapo zaidi ya Vijana 1,700 wamejitokeza kuomba nafasi hizo licha ya mahitaji kuwa ni madereva 1,500 pekee.

Akizungumza wakati wa ziara yake chuoni hapo tarehe 06 Februari 2026, Waziri wa Nchi hiyo Mhe. Clement Sangu, amesema Serikali imeweka mifumo imara ya kisheria inayosimamia Ajira hizo ili kulinda maslahi ya Watanzania.

Waziri Sangu pia amebainisha kuwa tangu mwezi Novemba 2025 hadi Januari 2026, jumla ya Watanzania 2,019 wameunganishwa na fursa za Ajira katika nchi za Saudi Arabia, Qatar, Oman, Falme za Kiarabu na kwingineko.

Aidha, amesema Serikali iko mbioni kusaini hati za makubaliano na nchi nyingine 16 ili kuzidi kutanua wigo wa Ajira kwa vijana.

Mhe. Sangu ametoa wito kwa vijana kuendelea kuchangamkia fursa hizo kupitia njia rasmi za Serikali na kuepuka mawakala wasio rasmi kwa maslahi ya usalama wao na Taifa kwa ujumla.

Akizungumza kwa niaba ya waombaji, mmoja wa madereva waliojitokeza, Hassan Mohamed, amesema ameamua kufuata utaratibu huo rasmi kwa kuwa unatoa uhakika wa ulinzi wa haki na maslahi yake akiwa ugenini.

Juhudi hizi zinaonyesha dhamira ya Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu katika kutengeneza mifumo inayotoa matumaini na usalama kwa nguvu kazi ya kitanzania inayotafuta fursa nje ya mipaka.

Mkurugenzi Mtendaji wa Jukwaa la Watendaji Wakuu nchini (CEO Roundtable of Tanzania-CEOrt) B. Santina Benson (kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Wanawake Wafanyabiashara Tanzania (TWCC) Dkt. Mwajuma Hamza  wasaini Hati ya Makubaliano (MoU) kwa ajili ya kushirikiana katika kuwawezesha wafanyabishara wanawake kukua kiuchumi kupitia mpango wa CEOrt unaojulikana kama ‘Think Equal, Lead Smart (TELS), ulioanzishwa mwaka 2024 kwa kushirikiana na Vodacom Tanzania Foundation.Hafla hiyo imefanyika katika hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam Ijumaa Februari 6, 2026
Mkurugenzi Mtendaji wa Jukwaa la Watendaji Wakuu nchini (CEO Roundtable of Tanzania-CEOrt) B. Santina Benson (kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Wanawake Wafanyabiashara Tanzania (TWCC) Dkt. Mwajuma Hamza, mara baada ya kusaini Hati za Makubaliano (MoU) kwa ajili ya kushirikiana katika kuwawezesha wafanyabishara wanawake kukua kiuchumi kupitia mpango wa CEOrt unaojulikana kama ‘Think Equal, Lead Smart (TELS), ulioanzishwa mwaka 2024 kwa kushirikiana na Vodacom Tanzania Foundation. Hafla hiyo imefanyika katika hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam Ijumaa Februari 6, 2026.

Meneja wa Vodacom Tanzania Foundation, Bi. Sandra Oswald, akisisitiza  jambo wakati wa mwendelezo wa mkutano wa program ya Jukwaa la Watendaji Wakuu nchini ( CEO Roundtable of Tanzania- CEOrt)  inayojulikana kama ‘Think Equal, Lead Smart (TELS), ilioanzishwa mwaka 2024 kwa kushirikiana na Vodacom Tanzania Foundation, kwa lengo la kukuza usawa wa fursa kwa wanawake katika uongozi, biashara na nafasi za maamuzi.

Na Mwandishi Wetu
JUKWAA  la Wakurugenzi Wakuu Tanzania (CEO Roundtable of Tanzania-CEOrt) na Chama cha Wanawake Wafanyabiashara Tanzania (TWCC) kwa pamoja wamesaini Hati ya Makubaliano (MoU) ili kurasimisha ushirikiano wa kimkakati unaolenga kuharakisha uongozi na ushiriki wa wanawake katika shughuli za kiuchumi hapa nchini.

Ushirikiano huo utatekelezwa kupitia mpango wa CEOrt unaojulikana kama ‘Think Equal, Lead Smart (TELS), ulioanzishwa mwaka 2024 kwa kushirikiana na Vodacom Tanzania Foundation, kwa lengo la kukuza usawa wa fursa kwa wanawake katika uongozi, biashara na nafasi za maamuzi.

Kupitia ushirikiano huu, CEOrt na TWCC zitafanya kazi kwa pamoja kuimarisha biashara za wanawake ,ikiwemo biashara ndogo, ndogo sana na za kati (MSMEs)—kwa kuwajengea wanawake ujuzi wa uongozi, biashara na matumizi ya teknolojia za kidijitali, kuongeza utayari wa kukua kifedha, na kushughulikia vikwazo katika kijamii vinavyokwamisha maendeleo yao kiuchumi.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo ya utiaji saini iliyofanyika katika Hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mtendaji wa CEOrt, Bi. Santina Benson, alisisitiza umuhimu wa kushughulikia changamoto za kimfumo zinazoendelea kuzuia ushiriki kamili wa wanawake katika masuala ya kiuchumi na uongozi.

“Think Equal, Lead Smart imebuniwa kuunganisha wajasiriamali wanawake na mifumo ya sera, uwekezaji na uongozi na ushirikiano huu kati ya CEOrt na TWCC unaimarisha uwezo wetu wa kuwasaidia wanawake wanaojihusisha na shughuli za kiuchumi katika mikoa mbalimbali na kuhakikisha wanawake wanajumuishwa kikamilifu katika mifumo ya maendeleo na uongozi wa Tanzania,” alisema .Santina

Hata hivyo alibainisha kuwa MoU hiyo itafungua njia za upatikanaji wa mitaji, masoko na ushauri wa kibiashara kupitia wanachama wa CEOrt na washirika wa kimkakati. Miunganisho hiyo inatarajiwa kuongeza fursa kwa wanawake kupata mitaji, kuingia katika minyororo ya thamani ya juu zaidi, na kunufaika na mwongozo wa kibiashara pamoja na mitandao ya sekta mbalimbali.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa TWCC, Dkt. Mwajuma Hamza, alisema kuwa ushirikiano huo unashughulikia changamoto halisi zinazowakabili wanawake wajasiriamali nchini.

“Wanachama wetu bado wanakabiliwa na changamoto za upatikanaji wa mitaji, masoko, ushauri wa kitaalamu na nafasi za maamuzi. Ushirikiano huu na CEOrt unatoa fursa za vitendo kwa wanawake kujenga biashara endelevu, kupata nafasi za uongozi na kushindana kikamilifu katika uchumi,” alisema.

Ushirikiano huo ulitanguliwa na kikao cha kwanza cha maarifa cha Think Equal, Lead Smart, kilichowakutanisha viongozi wa biashara, washirika wa maendeleo, watunga sera na wanawake wajasiriamali jijini Dar es Salaam.

Kikao hicho kilifanyika katika Hoteli ya Serena chini ya kaulimbiu “Mustakabali wa MSMEs Zinazoongozwa na Wanawake: Ushirikishwaji, Changamoto na Fursa. Lengo ni kuwawezesha wanawake wajasiriamali kushiriki kikamilifu katika ajenda ya maendeleo ya muda mrefu chini ya Dira ya Maendeleo ya Tanzania 2050 (DIRA 2050).

Jukwaa la TELS lilibuniwa kukuza ushiriki jumuishi wa kiuchumi kwa kuhimiza majadiliano kati ya sekta binafsi, taasisi za kifedha, watunga sera na MSMEs zinazoongozwa na wanawake. Kupitia ubadilishanaji wa maarifa na majadiliano yanayoongozwa na sera, mpango huu unalenga kuwaweka wanawake wajasiriamali kama wahimili muhimu wa mabadiliko ya kiuchumi nchini.

Akizungumza katika jukwaa hilo, Meneja wa Vodacom Tanzania Foundation, Sandra Oswald, alisisitiza umuhimu wa kujenga mifumo itakayowezesha biashara zinazoongozwa na wanawake kukua, kurasimishwa na kushindana kwa uendelevu.

“MSMEs zinazoongozwa na wanawake ndizo mhimili wa uchumi wa Tanzania, zikichangia kwa kiasi kikubwa ajira, kipato cha kaya na ubunifu wa ndani. Hata hivyo, bado zinakabiliwa na vikwazo vya kimfumo vinavyozuia ukuaji wao. Ili Tanzania ifikie malengo ya Dira ya 2050, wanawake wajasiriamali lazima wajumuishwe kikamilifu katika mkakati wa ukuaji wa uchumi wa taifa,” alisema.

Kikao hicho kilitoa fursa kwa wanawake wajasiriamali kueleza wazi changamoto wanazokumbana nazo, ikiwemo ukosefu wa mitaji nafuu, changamoto za matumizi ya teknolojia za kidijitali, vikwazo vya kisheria na kiutawala, upungufu wa masoko na mifumo dhaifu ya msaada wa biashara.

Sandra alieleza kuwa kuoanisha majadiliano ya TELS na Dira ya 2050 kunazitambua MSMEs zinazoongozwa na wanawake kama nguzo muhimu za mabadiliko ya kiuchumi, ubunifu na ukuaji jumuishi.

Ikiwa katika hatua kwanza katika mipango mbalimbali iliyopangwa katika utekelezaji wake, jukwaa la maarifa la Think Equal, Lead Smart litaendelea kuwakutanisha wadau kwa ajili ya kubadilishana mawazo yanayotekelezeka, suluhisho za vitendo na mikakati inayooana na sera za kitaifa. Vikao vijavyo vinatarajiwa kufanyika katika mikoa na sekta mbalimbali, vikisisitiza nafasi ya MSMEs zinazoongozwa na wanawake kama wachangiaji wakuu wa ustawi wa taifa.

Shirika la Wanawake katika Sheria na Maendeleo Barani Afrika (WiLDAF Tanzania), kwa kushirikiana na mtandao wa kupambana na ukatili wa kijinsia (Mkuki) na wadau wengine wa maendeleo, wameandaa na kugawa tuzo kwa vinara 16 wa kupinga vitendo vya ukatili wa kijinsia na utetezi wa haki za binadamu.


Ugawaji wa tuzo hizo umefanyika Februari 05, 2026 jijini Dar es salaam na kuhudhuriwa na wawakilishi wa serikali, mabalozi mbalimbali, mashirika ya Umoja wa Mataifa, wanaharakati wa haki za wanawake, wanasheria, vyombo vya habari na asasi za kiraia,


Akizungumza katika Hafla hiyo, Mkurugenzi wa WiLDAF Tanzania, Wakili Anna Kulaya, alisisitiza kuwa juhudi za kupambana na ukatili wa kijinsia kwa wanawake na watoto ni jukumu letu sote ikiwa ni Pamoja na kuwasaidia wote waliopitia ukatili huo. Huku akipongeza hatua ya jamii kubwa ambayo kwasasa haikalii kimya ukatili wa kijinsia kwa wanawake na watoto.

“Tumeona viongozi wa jamii wanabadili fikra na kuwa sehemu ya jitihada zetu za kuukata ukatili wa kijinsia hasa baadhi ya mila potofu. Tumeona kuongezeka kwa uelewa wa haki za kisheria na haki za binadamu kiujumla. Kwasasa wanajamii wengi wanavunja ukimya dhidi ya vitendo hivi, wanachukua hatua kudai haki na uwajibikaji”,amesema


Aidha, amepongeza juhudi za serikali katika kuunga mkono mapambano hayo ya uimarishwaji wa mifumo ya utoaji haki ikiwa ni Pamoja na kuongeza idadi ya madawati ya kijinsia, Pamoja na kuongezeka kwa weledi wa kuwahudumia waathirika na wahanga wa vitendo vya ukatili huo.


“Tumeona uimarishwaji wa mifumo ya utoaji haki ikiwa ni Pamoja na kuongeza idadi ya madawati ya kijinsia, Pamoja na kuongezeka kwa weledi wa kuwahudumia waathirika na wahanga wa vitendo vya ukatili huo”, ameongeza Kulaya.


Bi. Kulaya ametumia nafasi hiyo kuwashukuru wadau wa maendeleo waliounga mkono kufanikisha zoezi la ugawaji tuzo hizo ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha haki za wanawake na watoto, wadau hao ni Ubalozi wa Uswisi, Ubalozi wa Finland, ubalozi wa Ireland, UNFPA, UNICEF, LSF,BRAC, ITV, Coca-Cola Kwanza Ltd, na TBL.










































Top News