NA DENIS MLOWE,IRINGA

MBUNGE wa Jimbo la Iringa Mjini, Fadhili Ngajilo, amekabidhi msaada wa vifaa mbalimbali vya elimu kwa watoto wenye maisha duni wanaosoma katika shule za msingi mkoani Iringa, akisisitiza wazazi kuhakikisha watoto wote, wakiwemo wenye ulemavu, wanapata haki yao ya elimu.

Akizungumza katika hafla iliyofanyika katika Shule ya Msingi Ugele, Ngajilo alikabidhi magodoro, madaftari, mahindi, maharage, matranka na vifaa vingine muhimu vinavyolenga kuboresha mazingira ya kujifunzia na kuishi kwa watoto hao.

Ngajilo aliwataka wazazi kuacha tabia ya kuwaficha watoto wenye ulemavu majumbani, akisema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imejipanga kuhakikisha kila mtoto anapata fursa ya elimu bila ubaguzi.

Alisema watoto wenye ulemavu wana uwezo mkubwa wa kufanikiwa iwapo watapata elimu na malezi bora, akitoa mfano wa watu wenye ulemavu waliofanikiwa duniani na nchini, wakiwemo wabunge wanaowakilisha wananchi bungeni.

"Ninawasihi wazazi, msiwafiche watoto wenye ulemavu wapeleke shule kwa sababu huwezi kujua atakuwa nani kesho. Elimu ndiyo msingi wa mafanikio yao," alisema Ngajilo.

Aliwapongeza walimu wanaofundisha watoto hao kwa kujitolea na kuendelea kutekeleza majukumu yao licha ya changamoto mbalimbali zinazowakabili, akisema kazi yao ni wito unaohitaji moyo wa upendo na uvumilivu.

Ngajulo alieleza kuwa jukumu la viongozi ni kuweka mazingira bora ya watoto kupata elimu na huduma muhimu, huku akisisitiza kuwa malezi bora yanahitaji ushirikiano wa karibu kati ya wazazi na walimu.

Aliwataka wazazi kufuatilia maendeleo ya watoto wao hata wanaporudi nyumbani kwa kuwasaidia kufanya kazi za nyumbani (homework) ili kuongeza ufanisi katika kujifunza.

Ngajilo aliongeza kuwa ana matumaini kuwa kupitia uwekezaji katika elimu, Mkoa wa Iringa utaendelea kuzalisha wataalamu mbalimbali wakiwemo madaktari, wahandisi, maprofesa na viongozi watakaochangia maendeleo ya taifa.

Hafla hiyo ilihudhuriwa na viongozi wa serikali, walimu, wazazi na wanafunzi, huku msaada huo ukitarajiwa kusaidia kuboresha ustawi wa watoto wenye maisha duni na kuongeza fursa zao za kupata elimu bora.





NA DENIS MLOWE- MUFINDI, IRINGA

KAMATI ya Siasa ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Iringa ikiongozwa na Mwenyekiti wake, Daudi Yassin, imetembelea na kukagua utekelezaji wa miradi ya maendeleo yenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 23.6 katika Wilaya ya Mufindi, ikiwemo barabara ya kiwango cha lami ya Mtiri–Ifwagi pamoja na mtambo wa kuzalisha oksijeni tiba katika Hospitali ya Mji Mafinga.

Mradi mkubwa wa barabara ya Mtiri–Ifwagi wenye urefu wa kilomita 14 umegharimu shilingi bilioni 21.9, huku mradi wa mtambo wa kuzalisha oksijeni tiba katika Hospitali ya Mji Mafinga ukigharimu shilingi bilioni 1.78, fedha zilizotolewa kupitia Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa ushirikiano na washirika wa maendeleo.

Akiwasilisha taarifa ya mradi wa barabara, kwa. Kamati ya Siasa,Meneja wa Tarura Mkoa wa Iringa Injinia Davies Tembo alisema kuwa barabara hiyo ilijengwa chini ya Mradi wa RISE (Roads to Inclusion and Socioeconomic Opportunities), unaofadhiliwa na Benki ya Dunia kwa kushirikiana na Serikali ya Tanzania, kupitia Ofisi ya Rais-TAMISEMI na Wizara ya Ujenzi.

Alisema kuwa mradi huo ulianza Julai 27, 2023 na kukamilika Desemba 28, 2024, huku kipindi cha uangalizi wa mkandarasi (Defects Liability Period) kikimalizika Juni 30 mwaka huu.


Injinia Tembo alisema kuwa ujenzi wa barabara umehusisha kukata milima, kupasua miamba, kujenga madaraja mawili, makalavati 37, kuweka tabaka mbalimbali za barabara pamoja na kufunga taa za barabarani 90.

Aidha, maeneo yenye miteremko mikali yalijengwa kwa zege ili kuongeza uimara wa miundombinu hiyo na kukamilika kwa barabara hiyo kumerahisisha usafirishaji wa mazao ya misitu, chai, mboga mboga na mazao mengine ya biashara, kupunguza gharama za usafiri, pamoja na kuboresha upatikanaji wa huduma za kijamii ikiwemo afya, elimu na huduma za kiutawala kwa wananchi wa Ifwagi na maeneo jirani.

Kamati hiyo pia ilikagua mradi wa mtambo wa kuzalisha oksijeni tiba katika Hospitali ya Mji Mafinga uliotekelezwa kwa gharama ya shilingi bilioni 1,781,750,519.23 kupitia fedha za Serikali Kuu na Global Fund.

Mganga Mkuu wa halmashauri ya Mji Mafinga Dkt Bonaventula Chitopela akieleelezea kuwa mtambo huo una uwezo wa kuzalisha mitungi 60 ya oksijeni yenye ujazo wa lita 100 kwa siku na umeongeza kwa kiwango kikubwa ubora wa huduma za afya kwa wagonjwa wa dharura, wagonjwa wanaohitaji uangalizi maalumu (ICU), watoto wachanga pamoja na wajawazito.
Aidha, ulieleza kuwa kabla ya uwepo wa mtambo huo hospitali ilikuwa ikitumia wastani wa shilingi milioni tisa kununua oksijeni, lakini gharama hizo zimepungua hadi kufikia milioni nne kwa mwezi, hali inayookoa takribani shilingi milioni tano kila mwezi.

Hospitali hiyo pia imekuwa ikisambaza oksijeni tiba katika Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi, Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Iringa, Hospitali ya Manispaa ya Iringa, Hospitali ya Ipamba pamoja na vituo vingine vya kutolea huduma za afya.

Akizungumza baada ya kukagua miradi hiyo, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Iringa, Daudi Yassin, alisema Kamati ya Siasa imeridhishwa na ubora wa utekelezaji wa miradi hiyo kwani imeleta matokeo chanya kwa wananchi.

Alisema mradi wa mtambo wa oksijeni umeondoa changamoto ya upatikanaji wa huduma za dharura na kupunguza gharama za matibabu, huku barabara ya Mtiri–Ifwagi ikiwa imefungua fursa mpya za kiuchumi kwa wakazi wa Mufindi.

Yassin aliwataka wananchi kuendelea kuitunza miundombinu hiyo ili iweze kudumu na kuendelea kutoa manufaa kwa vizazi vya sasa na vijavyo.

Alisema utekelezaji wa miradi hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa Ilani ya CCM na kwamba wananchi wa Mufindi ni mashahidi wa ahadi zilizotekelezwa na serikali.

Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Ifwagi, Arafat Benson Mwambule, alimshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kupeleka fedha za ujenzi wa barabara hiyo, akisema tayari imeanza kuleta mabadiliko makubwa ya maendeleo katika eneo hilo na kwamba wananchi wana matarajio makubwa ya kuendelea kwa ujenzi wa kilomita nyingine zilizopangwa.

Naye Mwenyekiti wa Kijiji cha Ifwagi, Fransis Bilangulo, alisema barabara hiyo imebadilisha sura ya kijiji na kuongeza shughuli za maendeleo, akieleza kuwa wananchi wanaiona Ifwagi kuwa miongoni mwa maeneo yaliyonufaika zaidi na uwekezaji wa serikali katika miundombinu.

Ziara hiyo ya Kamati ya Siasa ya CCM Mkoa wa Iringa ni sehemu ya ukaguzi wa utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi pamoja na kutathmini maendeleo ya miradi inayotekelezwa na Serikali katika Wilaya ya Mufindi na itaendelea kesho kwa wilaya ya Iringa.




 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, ameishukuru Serikali ya Sweden kwa ushirikiano wake wa muda mrefu katika kuchangia maendeleo ya Zanzibar, huku akisisitiza umuhimu wa kuimarisha zaidi uhusiano wa pande hizo mbili kupitia biashara na uwekezaji.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, tarehe 14 Julai 2026, alipokutana na Balozi wa Sweden nchini Tanzania, Mhe. Charlotta Ozaki Macias, aliyefika Ikulu Zanzibar kwa ajili ya kumuaga baada ya kumaliza muda wake wa kazi nchini.

Aidha, Rais Dkt. Mwinyi amesema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeendelea kuweka mazingira rafiki na ya kuvutia uwekezaji katika sekta mbalimbali za kiuchumi, hususan nishati, uchumi wa buluu na kilimo cha mwani.

Ameeleza kuwa Serikali inakaribisha makampuni kutoka Sweden kuwekeza Zanzibar, hasa katika uzalishaji wa nishati mbadala ili kuongeza uzalishaji wa umeme na kuimarisha maendeleo ya uchumi.

Halikadhalika, Rais Dkt. Mwinyi amesema Serikali imejipanga kuongeza thamani ya zao la mwani kwa kulisindika na kuzalisha bidhaa mbalimbali, hatua itakayoongeza kipato cha wakulima na kuchochea ukuaji wa uchumi wa buluu.

Vilevile Rais Dkt.Mwinyi amesisitiza kuwa Zanzibar inaendelea kuthamini mchango wa Sweden katika sekta za elimu, afya na ustawi wa jamii, huku akiiomba nchi hiyo kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Zanzibar 2050.

Kwa upande wake, Balozi wa Sweden nchini Tanzania, Mhe. Charlotta Ozaki Macias, amempongeza Rais Dkt. Mwinyi na wananchi wa Zanzibar kwa hatua muhimu ya kuimarisha maridhiano ya kisiasa kupitia Tamko la Pamoja na utiaji saini wa Ajenda za Kuchukuliwa Hatua kati ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na ACT-Wazalendo.








 Na Benny Mwaipaja, Horohoro, Tanga

Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), ametoa wito kwa wafanyabiashara, wawekezaji na wazalishaji nchini kuongeza uzalishaji wenye tija na kuimarisha mauzo ya bidhaa katika masoko ya kimataifa ili kupunguza nakisi ya biashara (trade deficit) na kuongeza mchango wa sekta ya biashara katika kukuza uchumi wa Taifa.

Akizungumza wakati alipotembelea Kituo cha Huduma ya Pamoja Mpakani cha Horohoro, mkoani Tanga, ikiwa ni sehemu ya ziara yake mkoani humo, Mhe. Balozi Khamis alisema pamoja na mafanikio makubwa yaliyopatikana katika ukusanyaji wa mapato na uboreshaji wa mazingira ya biashara, bado ipo haja ya kuongeza thamani ya bidhaa zinazouzwa nje ya nchi ili Tanzania iweze kunufaika zaidi na biashara ya kimataifa.

Mhe. Balozi Omar alieleza kuwa takwimu za biashara kupitia Kituo cha Forodha cha Horohoro zinaonesha kuwa katika mwaka wa fedha uliopita bidhaa zenye thamani ya takribani shilingi bilioni 748 zilipitia katika kituo hicho, lakini kati ya hizo, bidhaa zilizouzwa nje ya nchi zilikuwa na thamani ya takribani shilingi bilioni 238 pekee, wakati bidhaa zilizoingizwa nchini zilifikia thamani ya shilingi bilioni 510, hali inayoonesha kuwepo kwa nakisi kubwa ya biashara.

"Matarajio ya kila taifa ni kuuza bidhaa nyingi zaidi kuliko linazoagiza kutoka nje, Takwimu hizi zinatuonesha bado tuna kazi kubwa ya kufanya katika kuongeza uzalishaji na kuimarisha mauzo ya bidhaa zetu nje ya nchi na Tanga ina fursa nyingi za uzalishaji na usafirishaji wa bidhaa, hivyo ni muhimu kuzitumia kikamilifu ili kupunguza nakisi hii," alisema Mhe. Balozi Khamis.

Alisisitiza kuwa Serikali itaendelea kuboresha mazingira ya biashara kupitia uwekezaji katika miundombinu ya forodha, mifumo ya kisasa ya ukaguzi wa mizigo pamoja na kuimarisha vituo vya mipakani ili kurahisisha biashara na kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania katika masoko ya kikanda na kimataifa.

Aidha, alisema mafanikio ya ukuaji wa uchumi yanatoa msingi mzuri wa kuongezeka kwa shughuli za biashara nchini, akibainisha kuwa uchumi wa Tanzania ulikua kwa asilimia 5.9 mwaka 2025 na unatarajiwa kukua kwa asilimia 6.3 mwaka 2026, jambo litakalochochea ongezeko la uzalishaji na biashara.

Kwa upande wa ukusanyaji wa mapato, Mhe. Balozi Khamis alisema Kituo cha Huduma ya Pamoja Mpakani cha Horohoro, kimewekewa lengo la kukusanya shilingi bilioni 136 katika mwaka wa fedha 2026/27, baada ya kuvuka matarajio ya mwaka uliopita kwa kukusanya shilingi bilioni 125, hivyo kutokana na mwenendo mzuri wa ukuaji wa uchumi na biashara, Serikali ina imani kuwa lengo hilo litafikiwa, huku akibainisha kuwa kituo hicho kinachangia karibu robo ya mapato yote yaliyopangwa kukusanywa katika Mkoa wa Tanga.

“Serikali imetenga shilingi bilioni 573 katika Bajeti ya mwaka 2026/27 kwa ajili ya kuendeleza maboresho ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), ikiwemo ununuzi wa scanners (midaki) 27 za kisasa zitakazowekwa katika vituo mbalimbali vya forodha nchini, ikiwemo Kituo cha Forodha cha Horohoro” alisema Mhe. Balozi Omar

Alieleza kuwa mchakato wa ununuzi wa vifaa hivyo tayari umeanza na unafanyika kwa kuzingatia taratibu zote za ununuzi wa umma, huku akieleza kuwa vifaa hivyo hutengenezwa kwa kuzingatia mahitaji maalumu ya kila kituo cha forodha, hivyo mchakato wake unahusisha usanifu, utengenezaji, ukaguzi wa ubora, usafirishaji na ufungaji kabla ya kuanza kutumika na uwekezaji huo utaongeza ufanisi wa ukaguzi wa mizigo, kuharakisha utoaji wa huduma, kuimarisha usalama wa mipaka na kuongeza usahihi katika ukusanyaji wa mapato ya Serikali.

"Hatununui tu vifaa vya kisasa, bali tunawekeza katika kuongeza ufanisi wa biashara, kuimarisha usalama wa nchi na kuhakikisha Serikali inapata mapato yake stahiki, ma Midaki hii itasaidia kujua kwa uhakika bidhaa zinazopita mipakani, kupunguza muda wa ukaguzi na kurahisisha biashara halali," aliongeza Mhe. Balozi Omar.

Aliwahimiza pia wafanyabiashara kuendelea kutumia Kituo cha Huduma ya Pamoja Mpakani cha Horohoro, kufanya biashara halali na kuongeza mauzo ya bidhaa za Tanzania katika masoko ya nje, akisisitiza kuwa hatua hiyo itaongeza mapato ya fedha za kigeni, kupunguza nakisi ya biashara (trade deficit) na kuimarisha uchumi wa nchi.

Naye Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Tanga ambaye pia ni  Mkuu wa Wilaya ya Tanga mjini, Mhe. Dadi Kolimba, alisema Mkoa wa Tanga unaendelea kuwa miongoni mwa mikoa inayoongoza nchini katika ukusanyaji wa mapato, ukiwa wa sita kitaifa, mafanikio ambayo yamechangiwa kwa kiasi kikubwa na utendaji mzuri wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) pamoja na ushirikiano wa taasisi nyingine za Serikali zinazofanya kazi katika vituo vya mipakani.

Alisema Kituo cha Forodha cha Horohoro ni miongoni mwa vituo muhimu vya kiuchumi vinavyochangia kwa kiwango kikubwa mapato ya Mkoa wa Tanga na Taifa kwa ujumla, akibainisha kuwa katika mwaka wa fedha uliopita kituo hicho kilivuka lengo lake kwa kukusanya shilingi bilioni 125 dhidi ya lengo la shilingi bilioni 115. Aliongeza kuwa Serikali ya Mkoa itaendelea kushirikiana na TRA kutatua changamoto zinazojitokeza, kuimarisha mazingira ya biashara na kuhamasisha uzalishaji pamoja na mauzo ya bidhaa za Tanzania katika masoko ya nje ili kuongeza mapato ya Serikali na kuchochea ukuaji wa uchumi.

Kwa Upande wao Naibu Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Bw. Mcha Hassan Mcha, na Afisa Mfawidhi wa Kituo cha Huduma ya Pamoja Mpakani cha Horohoro, Bw. Shadrack Mbonea, walisema kuwa wamejipanga vyema kupambana na Magendo kwa kuimarisha doria za kimkakati kwa kushirikiana na taasisi nyingine za Serikali.

Walibainisha kuwa wataendelea kuimarisha ukaguzi wa mizigo inayoingia na kutoka nchini ili kuhakikisha wanatokomeza magendo lakini pia kuihakikisha kodi stahiki inakusanywa.

Katika Ziara hiyo Mhe. Balozi Omar aliambatana pia na, Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha ambaye pia ni Mhasibu Mkuu wa Serikali, CPA Leonard Mkude, Makamishna na maafisa waandamizi kutoka Wizara ya Fedha pamoja na taasisi zake.










Mbunge wa Jimbo la Dodoma Mjini Mhe. Paschal Inyasi Chinyele, amesema Serikali inaendelea kutekeleza hatua mbalimbali za kuboresha huduma za kijamii katika Kata ya Zuzu, akibainisha kuwa eneo hilo ni miongoni mwa maeneo yanayokua kwa kasi hivyo linahitaji uwekezaji zaidi katika miundombinu ya msingi, hususan huduma ya maji.

Akizungumza katika mkutano wa hadhara wa kutoa changamoto na kero mbalimbali zinazowakabili wananchi kwa mkuu wa mkoa wa Dodoma Julai 13, 2026, uliofanyika eneo la Chididimo lililopo Kata ya Zuzu Halimashauri ya Jiji la Dodoma, amesema kupitia Mfuko wa Jimbo la Dodoma Mjini, licha ya kugawana fedha na Jimbo la Mtumba katika mwaka wa fedha uliopita.

Amesema waliweza kutenga shilingi milioni 20 kwa ajili ya kuchimba kisima cha maji katika Shule za Msingi Chang’ombe na Milioni 20 zingine walichimba kisima katika shule ya msingi Chididimo, huku fedha za ujenzi wa kibanda cha kisima zikiwa zimepatikana kupitia nguvu ya wananchi na Halmashauri ya Jiji la Dodoma inatarajia kukamilisha miundombinu iliyobaki.

Mbunge huyo amesema upatikanaji wa maji ni kipaumbele kwa kuwa hakuna maisha bila maji, akisisitiza kuwa mradi huo utawanufaisha wananchi kwa kiasi kikubwa, aidha amesema Serikali imetoa shilingi milioni sita kwa ajili ya ujenzi wa maabara katika Hospitali ya Nzinje na shilingi milioni 46 kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa shule ya sekondari, hatua itakayopunguza adha ya wanafunzi kutembea umbali mrefu na kukabiliwa na vihatarishi vinavyoweza kuathiri masomo yao ikiwemo utoro na mimba.

Awali, Diwani wa kata hiyo aliwasilisha changamoto zinazoikabili Zuzu na kuomba kukamilishwa kwa kipande cha barabara ya lami chenye urefu wa kilomita tano kinachoelekea Ring Road, ujenzi wa vivuko pamoja na soko la kisasa litakalowarahisishia wananchi kupata huduma za biashara karibu na makazi yao badala ya kutumia gharama kubwa za usafiri kufuata huduma hizo maeneo ya mbali.

Akizungumza katika ziara hiyo, Mstahiki Meya wa Jiji la Dodoma, Alimwoni Chaula, amepongeza utaratibu wa Mkuu wa Mkoa wa kutembelea wananchi na kusikiliza changamoto zao moja kwa moja, akisema hatua hiyo imeongeza kasi ya upatikanaji wa ufumbuzi wa kero mbalimbali na wananchi kuwa karibu na serikali Yao.

Amesema katika mwaka wa fedha 2026/2027, Jiji la Dodoma limetenga shilingi milioni 50 kwa kila eneo kwa ajili ya kujenga masoko katika maeneo yasiyo na huduma hiyo, huku Kata ya Zuzu ikiwa miongoni mwa maeneo yatakayonufaika, amesisitiza kuwa utekelezaji wa miradi hiyo utachochea maendeleo ya kiuchumi na kuboresha maisha ya wananchi wa Dodoma Mjini.












Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga (Mb), amemkabidhi mfanyabiashara mwenye ulemavu, Bi.Esther Mashaka Msengi, mashine ya kusagia viungo ili kuongeza uzalishaji, kupunguza gharama za biashara na kuboresha kipato chake.

Akikabidhi mashine hiyo katika Viwanja vya Maonyesho ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), amesema aliguswa na changamoto za Esther aliyekuwa akitumia muda na fedha nyingi kusafirisha viungo kwenda kusagwa kabla ya kuvifungasha na kuviuza.

Amesema Serikali itaendelea kushirikiana na taasisi zake kuhakikisha anaimarisha biashara yake, huku akiitaka BRELA kukamilisha usajili wa nembo ya bidhaa zake, TBS kumsaidia kupata ithibati ya ubora na SIDO kuendelea kumjengea uwezo.

Aidha, amelishukuru Shirika la Uhandisi na Usanifu Mitambo Tanzania TEMDO kwa kuwezesha upatikanaji wa mashine hiyo na kueleza kuwa hatua hiyo inaunga mkono maono ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuwawezesha wajasiriamali kuongeza tija.

Kwa upande wake, Bi. Esther Msengi amesema mashine hiyo itapunguza gharama za uzalishaji na kumwezesha kupanua biashara yake.

Mwakilishi wa Shirika la Uhandisi na Usanifu Mitambo Tanzania (TEMDO), Mhandisi. Elisante Mjema, amesema mashine hiyo inaweza kusaga kilo 10 za viungo kwa saa moja na kuongeza uzalishaji hadi kufikia mauzo ya takribani shilingi milioni 1.5 kwa siku endapo kutakuwa na malighafi za kutosha.

NA MWANDISHI WETU

Mwenyekiti Taifa wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT), Mary Chatanda, amemshauri aliyewahi kuwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Prof. Anna Tibaijuka, kuwa balozi wa kuhimiza viongozi na wananchi kutii sheria za nchi ili kuepuka kuingia katika mikono ya vyombo vya sheria.

Chatanda ameyasema hayo Julai 14, 2026, kufuatia ujumbe alioandika Prof. Tibaijuka katika Mtandao X, kuhusiana na kesi inayomkabili Mwenyekiti Taifa wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Tundu Lissu.

Katika ujumbe wake, Prof. Tibaijuka amesema "Dkt. Samia Suluhu, Mhe. Rais naendelea kushauri kwa dhati Tundu Lissu aachiwe huru kwani kesi haikamiliki, hekima na busara iliyotufanya kuitangaza sera ya 4Rs ulipoingia madarakani ikuongoze tena katika jambo hili".

"Simulizi hizi za kutisha za vyombo vya habari vya kimataifa zinainua hisia kali hasa kwa vijana, hata wazee tumekumbushwa kadhia ya operation Sogeza na iliyounda Vijiji vya Ujamaa 1974-1976, taarifa hizi zinaathiri kikubwa taswira ya Taifa letu na maslahi yake, athari ni kubwa".

"Tutafute muafaka kupitia uwajibikaji na maridhiano, tuwe na hofu ya Mungu na kutambua miujiza yake mfano wa risasi 16 kushindwa kukomesha uhai ingawa maumivu ni makubwa, tutubu na kusali kuliombea Taifa letu kila mtu kwa imani yake," ameongeza Prof. Tibaijuka katika andiko lake hilo.

Kutokana na andiko hilo, Chatanda amesema nchi inaongozwa kwa mujibu wa sheria na ni vyema mahakama iachwe ifanye kazi yake ili haki itendeke.

"Tusiruhusu utamaduni wa jambo linapokuwa mahakama, basi tuanze kumshinikiza Rais aingilie kati na kulimaliza. Tuiache mahakama ifanye kazi yake, na pale itakapothibitika kuwa mtuhumiwa hana hatia, basi ataachiwa huru," amesema Chatanda.

Sambamba na hilo, amesema, Tanzania ni nchi huru yenye mamlaka kamili na inaendesha mambo yake kwa mujibu taratibu zilizopo, hivyo hata vyombo vya habari vya kimataifa vinapaswa kuheshimu taratibu zetu za uendeshaji wa nchi na mashauri ya kisheria.

"Tusiruhusu kila kinachoandikwa katika vyombo vya habari vya kimataifa kikayumbisha na kusababisha kuacha kusimamia sheria za nchi, ni lazima tuheshimiane linapokuja suala la utii wa sheria za nchi," amesema.

Sanjari na hilo, Chatanda amesema, mataifa yaliyoendelea ni watii wazuri wa sheria zao, hivyo na sisi Watanzania tuwe na utamaduni wa kuheshimu sheria na mamlaka zilizopo na kutambua kuwa kamwe maridhiano si mbadala wa uvunjifu wa sheria.

"Dhana ya maridhiano isitumike vibaya, Rais Dk. Samia Suluhu Hassan amekuwa kinara wa maridhiano na hata alivyoingia madarakani aliwarejesha viongozi wa upinzani waliokuwa nje ya nchi, akawakaribisha warudi nyumbani ili nao watoe mchango wao katika ujenzi wa taifa, lakini baadhi yao ndo wamekuwa vinara wa kutoa kauli za kebehi na dharau kwa viongozi na serikali, hivyo tunapohimiza maridhiano, tusisahau pia utii wa sheria," amesema.

Katika hatua nyingine, Chatanda ametoa wito kwa wananchi kuendelea kuheshimu sheria za nchi ili kuepuka mkono wa sheria kwani nchi yetu inaongozwa kwa kuzingatia utawala wa sheria. Pia, amesisitiza umuhimu wa wananchi kulinda amani kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.



Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule, amewataka wazazi na walezi kujinyima mahitaji mengine ili kuhakikisha watoto wao wanapata elimu, akisisitiza kuwa elimu ndiyo msingi wa mafanikio katika dunia ya sasa inayohitaji watu wenye ujuzi na maarifa.

Akizungumza katika mkutano wa hadhara wa kusikiliza kero za wananchi uliofanyika Julai 13, 2026 katika eneo la Chididimo, Kata ya Zuzu, Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Senyamule amewapongeza wananchi wa kata hiyo kwa kuendelea kuboresha sekta ya elimu.

Amesema Shule ya Sekondari Zuzu, ambayo awali ilikuwa ya mwisho kimkoa kwa ufaulu, sasa imepanda hadi nafasi ya tisa kimkoa, jambo alilolitaja kuwa ni mafanikio makubwa.

Amesema mafanikio hayo yametokana na ushirikiano wa walimu, wazazi, wanafunzi na wadau wengine wa elimu, huku akisisitiza kuwa walimu hawawezi kufanikisha ufaulu bila wazazi kutekeleza wajibu wao wa kuhakikisha watoto wanahudhuria masomo kila siku.

Senyamule amesema Mkoa wa Dodoma umeendelea kufanya vizuri kitaifa katika elimu ya msingi kwa kushika nafasi ya pili, huku ukilenga kufikia nafasi ya kwanza kupitia ushirikiano wa karibu kati ya serikali, walimu na jamii.

Aidha, amewataka wazazi kuendelea kuiunga mkono serikali ambayo imewekeza katika ujenzi wa madarasa na miundombinu ya elimu, kwa kuhakikisha watoto hawakosi shule, amesema elimu si jambo la kusubiri bali ni uwekezaji unaoleta matokeo ndani ya muda mfupi.

Ameeleza kuwa watoto wanaopata elimu leo ndiyo watakaokuwa nguzo ya maendeleo ya vijiji, mitaa na kata katika miaka ijayo, kupitia maarifa na ujuzi watakaoupata shuleni.

Senyamule amesema zamani mtu aliweza kuishi bila elimu na akaendelea na maisha, lakini kwa kizazi cha sasa na kijacho hali hiyo haitakuwa rahisi kutokana na ongezeko la mahitaji ya wataalamu katika sekta mbalimbali, amesisitiza kuwa ni wajibu wa kila mzazi kuhakikisha mtoto anapata elimu ili aweze kushindana na kukabiliana na mahitaji ya dunia ya kisasa.






Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imekuletea mashindano ya Wazo Bunifu yanayolenga kupata suluhisho za kibunifu zitakazochangia kuboresha mfumo wa kodi nchini. Hii ni fursa yako ya kuwasilisha wazo lenye tija na kushindania zawadi ya hadi Shilingi Milioni 50.

Mawazo yatakayowasilishwa yanapaswa kulenga eneo moja au zaidi kati ya yafuatayo ; kupanua wigo wa kodi, kurahisisha ukadiriaji na ulipaji wa kodi kwa biashara ndogo ndogo, kuimarisha huduma za kodi za kidijitali, kupunguza gharama za ukusanyaji wa mapato, kutumia teknolojia za kisasa kama AI, Big Data na Blockchain katika usimamizi wa kodi, pamoja na kuboresha utatuzi wa migogoro ya kodi ili kuwa wa haraka, wazi na wenye kuaminika zaidi.

Kutuma Wazo lako ingia tovuti ya TRA, Bonyeza kitufe cha innovation portal fuata hatua zinazofuata, Mwisho wa kutuma wazo lako bunifu ni julai 31, 2026.

MWISHO WA SHINDANO HILI NI MWEZI HUU WA 7 NI HATARII


Kote nchini Tanzania, baa zina nafasi muhimu katika maisha ya kila siku ya jamii. Ni maeneo ambako marafiki hukutana, majirani hujumuika, mashabiki wa soka hutazama mechi pamoja, na biashara ndogo hukua.

Kupitia kampeni yake ya Cheers to Bars, Kampuni ya Tanzania Breweries Public Limited Company (TBL) inazitambua na kuzisherehekea baa kwa mchango wao katika kuwaleta watu pamoja na kusaidia uchumi mpana. Mbali na kuwa sehemu ambayo wateja hufurahia vinywaji, baa pia hutoa ajira kwa wamiliki, wahudumu, mabaa, wauzaji wa chakula, wasambazaji, wasafishaji, walinzi na watoa huduma za usafiri.

Kampeni hii pia inaangazia jinsi baa zinavyokuwa na umuhimu mkubwa zaidi wakati wa matukio makubwa ya michezo. Kadri hamasa ya soka inavyoendelea kuongezeka, mashabiki wengi huchagua kutazama mechi kwenye baa kwa sababu uzoefu huo huwa wa kuvutia zaidi unaposhirikishwa na wengine.

Katika Baa ya Kitambaa Cheupe jijini Dar es Salaam, mashabiki walikusanyika kushuhudia mechi ya robo fainali kati ya Hispania na Ubelgiji. Mechi hiyo ilikuwa mfano halisi wa jinsi baa za kienyeji zinavyobadilisha matukio ya soka ya kimataifa kuwa uzoefu wa pamoja wa kijamii. Mashabiki walitazama mchezo pamoja, wakashangilia, wakashiriki hisia na kuunda kumbukumbu za pamoja.

TBL inasema kuwa Cheers to Bars si kampeni inayohusu soka pekee. Ni kampeni inayotambua watu na biashara zinazowezesha maeneo ambayo yanaufanya mchezo wa soka kuwa sehemu ya maisha ya jamii.

"Baa ni sehemu muhimu ya maisha ya kijamii na kiuchumi ya Watanzania. Zinasaidia kujenga maisha ya watu, zinatoa fursa kwa biashara ndogo ndogo na zinatoa nafasi kwa jamii kukutana na kuimarisha mahusiano. Kupitia Cheers to Bars, tunazisherehekea baa hizi pamoja na watu wanaoziendesha, huku tukiwahamasisha watumiaji kufurahia vinywaji kwa kuwajibika," alisema Neema Temba, Mkurugenzi wa Sheria na Masuala ya Ushirika wa TBL.

Wakati wa mechi kubwa, baa yenye shughuli nyingi inaweza kunufaisha biashara zaidi ya moja. Wauzaji wa chakula, wasambazaji, watoa huduma za usafiri na timu mbalimbali za huduma zote hunufaika kutokana na ongezeko la shughuli. Hii inaifanya baa kuwa sehemu muhimu ya mfumo wa sekta ya ukarimu na burudani.

Mashabiki walipokusanyika katika baa ya Kitambaa Cheupe, mechi kati ya Hispania na Ubelgiji ilionyesha jinsi soka linavyowaunganisha watu na jinsi baa za kienyeji zinavyochangia kuunda uzoefu huo wa pamoja.

TBL inaendelea kuwahamasisha watumiaji kusherehekea kwa kuwajibika, kuunga mkono baa za kienyeji na kufurahia matukio ya soka katika mazingira salama na yenye furaha.

Kampeni ya Cheers to Bars ni ukumbusho kwamba baadhi ya kumbukumbu bora zaidi za soka hazitengenezwi uwanjani pekee. Pia huundwa katika baa za mitaani, ambako jamii hukusanyika, biashara hustawi na watu hushirikiana kufurahia mchezo.


















Top News