Na Pamela Mollel, Arusha

Habari njema kwa wakazi wa Arusha! Halmashauri ya Wilaya ya Arusha imependekeza bajeti ya shilingi bilioni 75.4 kwa mwaka wa fedha ujao, hatua inayotajwa kuwa chachu ya maendeleo katika sekta mbalimbali ikiwemo elimu, miundombinu na huduma za kijamii.

Bajeti hiyo inatajwa kuwa na neema kubwa kwa wanafunzi wapya zaidi ya 20,000 wanaotarajiwa kujiunga na kidato cha kwanza mwakani.

Akizungumza katika kikao cha Baraza la Madiwani kilichofanyika juzi, Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo, Baraka Simon, alisema bajeti hiyo imegawanyika katika sehemu kuu mbili.

Alifafanua kuwa kati ya bilioni 75.4 zilizopendekezwa, fedha hizo zimeelekezwa katika miradi ya maendeleo, huku mapato ya ndani yakitarajiwa kuwa shilingi bilioni 9.2.

“Bilioni 75.4 ni kwa ajili ya miradi ya maendeleo, lakini kwa upande wa mapato ya ndani ni bilioni 9.2. Tuna imani kubwa sana na bajeti hii na tunajua italeta mafanikio makubwa sana na itakuwa rafiki kwa wananchi,” alisema.

Katika hatua nyingine, alisema bajeti hiyo imelenga pia kuandaa vyumba zaidi ya 200 vya madarasa kwa ajili ya wanafunzi wapya wa kidato cha kwanza watakaoanza masomo mwakani.

Alieleza kuwa mabadiliko yanayotarajiwa katika mfumo wa elimu yataongeza idadi ya wanafunzi wa kidato cha kwanza, baada ya wanafunzi wa darasa la sita kuhitimu na kujiunga na ngazi hiyo sambamba na wenzao wengine.

“Mwakani kutakuwa na mabadiliko ya mfumo wa elimu. Wanafunzi wa darasa la sita wakimaliza watajiunga na kidato cha kwanza, lakini hata hao wengine nao wanatakiwa kuingia kidato cha kwanza. Tumejipanga vyema,” aliongeza.

Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Mlangarini, Emanuel Mrema, alisema wanashukuru kwa bajeti hiyo kwani imegusa nyanja zote muhimu zinazohitajika katika jamii.

Alisema pamoja na kuwepo kwa changamoto katika baadhi ya kata, kupitia bajeti hiyo vijiji vyote vitanufaika na miradi ya maendeleo itakayotekelezwa katika mwaka wa fedha ujao.

Kwa ujumla, bajeti hiyo imeibua matumaini mapya kwa wananchi wa Wilaya ya Arusha, huku matarajio makubwa yakiwekwa katika utekelezaji wake ili kuleta matokeo chanya yanayokusudiwa.



 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano), Deus Sangu, akiwasilisha hotuba yake mbele ya wajumbe wa Kamati ya Ulinzi na Usalama na Mkoa wa Geita, Menejimenti ya Mgodi wa Geita na watendaji wa Ofisi yake katika ziara ya kufuatilia utekelezaji wa Sheria ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi na Sheria nyingine za kazi katika Mgodi wa Dhahabu wa Geita (GGML).

*************

Na Mwandishi Wetu

Wito umetolewa kwa makampuni makubwa ya uchimbaji madini nchini kuwekeza katikakuwawezesha wachimbaji wadogo katika nyanja mbalimbali ikiwemo teknolojia za kisasa na usimikaji wa mifumo ya usalama na afya mahali pa kazi ili kujenga uchumijumuishi unaotokana na sekta ya madini.

Wito huo umetolewa na serikali kupitia Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano), Deus Sangu, alipofanya ziara ya kufuatilia utekelezaji wa Sheria yaUsalama na Afya Mahali pa Kazi na Sheria nyingine za kazi katika Mgodi wa Dhahabuwa Geita (GGML).

Waziri Sangu ameipongeza menejimenti ya Mgodi huo kwa kuzalisha ajira nyingi kwaWatanzania ambapo GGML imeajiri jumla ya wafanyakazi 2,366 moja kwa moja na4,629 wameajiriwa kupitia wakandarasi mbalimbali wanatoa huduma katika Mgodi waGGML.

Sambamba na pongezi hizo, Waziri mwenye dhamana ya masuala ya kazi ameutakaMgodi huo kuhakikisha kwamba shughuli zake zinakuwa na athari chanya katikauchumi wa jamii zinazowazunguka kwa kutoa fursa za kazi za muda mfupi ikiwemokuwezesha miradi mbalimbali ya kijamii.

Aidha, Waziri Sangu ameipongeza GGML kwa kuchagua suala la usalama na afya kwawafanyakazi kuwa tunu yao ya kwanza katika shughuli zao za uchimbaji na uchakatajiwa madini jambo ambalo limewafanya kujenga mifumo madhubuti ya kulinda afya nausalama wa wafanyakazi inayozingatia matumizi ya teknolojia za kisasa.

“Ninawapongeza kwa kuweka usalama na afya kama tunu yenu ya kwanza na hiiimejidhirisha katika wasilisho lenu mlilofanya hapa ambapo masuala ya usalama naafya yamechukua nafasi ya juu zaidi ya biashara mnayofanya,” ameeleza Waziri Sangu na kuongeza:

“Pongezi hizi inastahili pia Taasisi ya OSHA ambayo imekuwa ikiwaongoza katikakutekeleza hayo kupitia usimamizi mzuri wa Sheria Na.5 ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi ya mwaka 2003 na miongozo mbalimbali chini ya sheria hiyo ambayowamekuwa wakiitoa kupitia kaguzi zao za mara kwa mara.”

Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa katika ziara hiyo, Mkuu wa Wilaya ya Geita,Hashim Abdallah Komba, amesema OSHA ni miongoni mwa Taasisi zenye msaadamkubwa katika kuwezesha shughuli mbalimbali za kiuchumi kufanyika kwa tija katikaMkoa wa Geita.

Kwa upande wake Mtendaji Mkuu wa OSHA, Bi. Khadija Mwenda, amesema ziara hiyo, inalenga kuona jinsi OSHA inavyoshirikiana na wadau wake kutekeleza Sheria yaUsalama na Afya mahali pa kazi ambayo dhima yake kuu ni kulinda nguvukazi ya Taifa dhidi ya ajali na magonjwa yatokanayo na kazi pamoja na kulinda uwekezaji kupitiakuzuia uharibifu wa mali.

Awali, menejimenti ya GGML iliwasilisha taarifa juu ya shughuli zao iliyoainisha jinsiafya na usalama wa wafanyakazi unavyozingatiwa katika shughuli husika. Miongonimwa masuala yaliyoelezwa katika taarifa hiyo ni pamoja na historia ya mgodi ambapoimeelezwa kuwa madini katika mgodi huo yaligunduliwa mnamo mwaka 1898 nauchimbaji rasmi kuanza mwaka 1999.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano), Deus Sangu, akiwasilisha hotuba yake mbele ya wajumbe wa Kamati ya Ulinzi na Usalama na Mkoa wa Geita, Menejimenti ya Mgodi wa Geita na watendaji wa Ofisi yake katika ziara ya kufuatilia utekelezaji wa Sheria ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi na Sheria nyingine za kazi katika Mgodi wa Dhahabu wa Geita (GGML).
Wajumbe wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Geita, Menejimenti ya Mgodi wa Geita na watendaji wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano) wakifuatilia hotuba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano), Deus Sangu katika ziara ya kufuatilia utekelezaji wa Sheria ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi na Sheria nyingine za kazi katika Mgodi wa Dhahabu wa Geita (GGML).

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano), Deus Sangu, akiwa ameambatana na watendaji katika Ofisi yake na wajumbe wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Geita, wakifuatilia wasilisho la taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya Mgodi wa Dhahabu wa Geita (GGML) katika ziara ya kufuatilia utekelezaji wa Sheria ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi na Sheria nyingine za kazi katika Mgodi huo.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano), Deus Sangu, akiwa ameambatana na Mtendaji Mkuu wa OSHA, Bi.Khadija Mwenda, Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Geita na watendaji wengine katika Ofisi yake wakitembelea baadhi ya maeneo ya Mgodi wa Dhahabu wa Geita (GGML) katika ziara ya kufuatilia utekelezaji wa Sheria ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi na Sheria nyingine za kazi katika Mgodi huo. Katika ziara hiyo, wafanyakazi wa GGML walionesha onesho la jinsi wanavyochukua tahadhari dhidi ya vihatarishi mbalimbali vya ajali na magonjwa katika shughuli zao za kila siku.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano), Deus Sangu, akiagana na Mkurugenzi Mtendaji wa Mgodi wa Dhahabu wa Geita (GGML), Bw. Ashraf Suryaningrat, mara baada ya kuhitimisha ziara ya kufuatilia utekelezaji wa Sheria ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi na Sheria nyingine za kazi katika Mgodi huo.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano), Deus Sangu, akifanya majumuisho mara baada ya kuhitimisha ziara ya kufuatilia utekelezaji wa Sheria ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi na Sheria nyingine za kazi katika Mgodi wa Dhahabu wa Geita (GGML).
Mtendaji Mkuu wa OSHA, Bi.Khadija Mwenda akiwa na Meneja wa OSHA Kanda ya Ziwa, Lodgard Bishanga na Meneja Mwandamizi wa Usalama na Afya wa Mgodi wa Dhahabu wa Geita (GGML), Dr. Kiva Mvungi katika ziara ya kufuatilia utekelezaji wa Sheria ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi na Sheria nyingine za kazi GGML iliyofanywa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano), Deus Sangu.


Na Mwandishi Wetu Wetu - DODOMA


Wakala wa Vipimo Tanzania (WMA) imetoa mafunzo ya vipimo kwa wanafunzi wa Dr. Samia Dodoma Secondary School, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa vipimo sahihi katika biashara na maisha ya kila siku.

Katika zoezi hilo, wanafunzi walipata fursa ya kujifunza kuhusu dhima na majukumu ya Wakala huo, pamoja na namna unavyolinda maslahi ya watumiaji na wafanyabiashara kwa kuhakikisha vipimo vinakuwa sahihi na vya kuaminika.

Akizungumza baada ya mafunzo hayo, Meneja Mawasiliano na Uhusiano wa WMA, Veronica Simba, amesema elimu ya vipimo itatolewa katika mikoa yote ya Tanzania Bara ili kuhakikisha wanafunzi wengi zaidi wanapata uelewa wa matumizi sahihi ya vipimo.

Amesema mpango huo unalenga kukuza uelewa wa masuala ya vipimo kwa vijana, sambamba na kuimarisha utamaduni wa uadilifu na uwajibikaji katika sekta ya biashara nchini.

Kwa upande wake, Meneja wa Wakala wa Vipimo Mkoa wa Dodoma, Said Ibrahim, amesema mafunzo hayo yanaenda sambamba na uanzishwaji wa Klabu za Vipimo mashuleni ili kuendelea kuandaa mabalozi mahiri watakaotoa elimu ya vipimo shuleni na katika jamii kwa ujumla.

“Kwa Dodoma tayari tumeshatoa mafunzo katika shule mbili ambazo ni Shule ya Msingi Mtemi Mazengo na leo tumetoa hapa katika Shule ya Sekondari ya Dkt. Samia Dodoma. Tunaamini mabadiliko katika matumizi ya vipimo sahihi yataongezeka,” amesema Said.

Naye , Mwalimu Mussa Madandi, ambaye pia ni mlezi wa Klabu ya Vipimo shuleni hapo, amesema elimu hiyo wamekuwa wakiifundisha darasani, lakini mafunzo yaliyotolewa na WMA yamewapa wanafunzi nafasi ya kujifunza kwa vitendo, jambo litakalosaidia kuongeza uelewa na kuimarisha matumizi ya vipimo sahihi.

“Vipimo ni somo tunalolifundisha karibu kila darasa, lakini leo wanafunzi wamepata mafunzo kwa vitendo kutoka kwa wataalamu wenyewe. Naamini hali hii itaongeza hamasa ya kuzingatia usahihi katika matumizi ya vipimo na kuwafanya wawe mabalozi wazuri kwa wazazi wao na jamii inayowazunguka,” amesema Mwalimu Madandi.

Mwanafunzi Itabangola Elias amesema elimu hiyo imewasaidia kuelewa namna ya kutambua vipimo sahihi na kujikinga dhidi ya udanganyifu unaoweza kujitokeza katika biashara.

Baada ya mafunzo hayo, wanafunzi walishiriki kujibu maswali mbalimbali kuhusiana na vipimo na shughuli za Wakala huo, ambapo waliofanya vizuri walipatiwa zawadi mbalimbali kama sehemu ya kuwahamasisha kuendelea kujifunza na kuwa mabalozi wa matumizi sahihi ya vipimo katika jamii.





-Ammwagia sifa Rais Dkt Samia kwa Mapinduzi ya elimu


NA MWANDISHI WETU, MBEYA

MKUU wa Wilaya ya Mbeya, Mhe. Solomon Itunda, amewataka wahitimu wa kidato cha sita nchini kuwa mabalozi wa nidhamu na uzalendo, huku akibainisha kuwa uwekezaji mkubwa unaofanywa na Serikali ya Awamu ya Sita ni dhamira ya dhati ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kutengeneza taifa la wasomi wenye ushindani.

Mhe. Itunda ameyasema hayo jana wakati akimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Mhe. Beno Malisa, katika mahafali ya kuwaaga wanafunzi wa kidato cha sita wa Shule ya Sekondari Ivume yaliyofanyika jijini Mbeya.


Sifa kwa Rais Samia na Maboresho ya Miundombinu

Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa, DC Itunda amempongeza kwa dhati Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kumwaga mabilioni ya fedha mkoani Mbeya kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa miundombinu ya elimu ikiwemo madarasa, maabara za kisasa na mabweni.

"Chini ya uongozi mahiri wa Mheshimiwa Rais Samia, tumeshuhudia mabadiliko makubwa ya mazingira ya kufundishia na kujifunzia. Serikali imekuwa ikitoa fedha kwa wakati ili kuhakikisha watoto wetu wanasoma katika mazingira bora, jambo ambalo limeongeza morali kwa walimu na kuinua kiwango cha ufaulu," alisema Mhe. Itunda.

Wito wa Nidhamu na Uzalendo kwa Wahitimu

DC Itunda amewahimiza wahitimu hao wa Ivume Sekondari kutolewa macho na mafanikio ya muda mfupi, badala yake wazingatie nidhamu na uzalendo wanapoelekea kwenye ngazi za juu za elimu. Aliwasisitiza kuwa Serikali inawategemea kama nguvu kazi ya baadae ya Taifa.

"Nidhamu ndiyo dira ya mafanikio yenu kuanzia sasa. Tunatarajia muwe mabalozi wazuri wa Ivume na Mkoa wa Mbeya kwa ujumla kule mwendako. Epukeni vitendo vinavyoweza kuharibu mustakabali wenu na wa Taifa lenu," aliongeza.

Maagizo kwa Waliobaki Shuleni

Kwa upande mwingine, Mhe. Itunda amewataka wanafunzi wanaoendelea na masomo kuongeza bidii na kuzingatia maadili mema, akionya kuwa Serikali haitasita kuchukua hatua dhidi ya yeyote atakayejihusisha na vitendo vya utovu wa nidhamu ambavyo vinakwamisha juhudi za kuinua taaluma.

Mapema, Uongozi wa Shule ya Sekondari Ivume uliishukuru Serikali ya Mkoa na Wilaya kwa ushirikiano wa karibu, ukiahidi kuendelea kusimamia taaluma na kulea vijana katika misingi ya uzalendo na uwajibikaji.





Tarehe 21 Februari 2026, 

Katika kuelekea kilele cha maadhimisho ya miaka 25 ya Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC), Kampasi ya Tabora imefanya ziara ya kijamii katika Kituo cha Kulelea Wazee wenye Mahitaji Maalum kilichopo Ipuli, Manispaa ya Tabora. Ziara hiyo ilikuwa ni sehemu ya mikakati ya chuo kuimarisha ushirikiano na jamii.

Katibu Tawala wa Wilaya ya Tabora, Bi. Asha Churu, kwa kushirikiana na Mkurugenzi wa Kampasi ya Tabora, Dkt. Joseph Mbwillo, wameongoza timu  ya watumishi na wanachuo wa Kampasi ya Tabora kutembelea kituo hicho katika kujali na kusaidia wazee wenye mahitaji maalum.

Lengo kuu la ziara lilikuwa ni kuwapelekea misaada mbalimbali kwa wahitaji hao, ikiwa ni pamoja na mchele, maharage, mafuta ya kupikia na mafuta ya kujipaka, sabuni za kuogea na kufulia, nguo, sukari, mashuka pamoja na nguo katika kuboresha maisha ya wazee hao.

Pamoja na kutoa misaada hiyo, timu hiyo pia ilifanya kazi ya usafi wa mazingira ya makazi ya wazee pamoja na  zoezi la upandaji miti katika eneo hilo kwa lengo la kuimarisha ustawi wao na kuhifadhi mazingira kwa ujumla.

Ziara hii ni sehemu kuelekea kilele cha maadhimisho ya mika 25 ya chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania kwa kuonyesha mfano wa jamii inayojali na kuendeleza mazingira kwa manufaa ya wote.








 

 MAMLAKA ya Uteuzi imeongeza muda wa siku arobaini na mbili (42) kuanzia tarehe 20 Februari, 2026 Tume ya Kuchunguza Matukio ya Uvunjifu wa Amani Wakati na Baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025 ili Tume iweze kukamilisha uchunguzi wa matukio ya uvunjifu wa amani ya wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa tarehe 29 Oktoba, 2025 na kuitaka ikamilishe kazi na kuwasilisha Taarifa yake kabla au ifikapo tarehe 3 Aprili, 2026. 

Kwa mujibu wa taarifa hiyo iliyotolewa katika gazeti la serikali Tume imeongezewa muda huo ili kutoa fursa na muda wa kutosha kwa kila mwenye taarifa, ushahidi au maoni, aliyepo nchini au nje ya nchi, kuwasiliana na Tume ili kuhakikisha kuwa hakuna mtu yeyote, au taasisi yoyote, itakayokosa nafasi ya kusikilizwa. 

Sababu nyingine za kuongeza muda ni pamoja na zifuatazo Wingi na mchanganyiko wa taarifa zilizokusanywa, na zinazoendelea kukusanywa, na Tume ambazo zinahitaji muda zaidi wa kufanyiwa uchambuzi wa kina, Tume kulazimika kutumia Wataalamu (experts) kutoka ndani na nje ya nchi wenye uwezo wa kufanya uchunguzi wa kisayansi, na uchambuzi wa kidijitali wa baadhi ya taarifa na vielelezo kutokana na aina ya matukio na ushahidi uliokusanywa hadi sasa, na unaoendelea kuwasilishwa.

Sababu nyingine ni Tume kubaini mapengo kadhaa katika taarifa na vielelezo vilivyokusanywa hadi sasa hivyo kuhitaji kutafuta au kupata taarifa zaidi ili kukamilisha ushahidi kwa kila hoja inayohusika, Kutoa fursa kwa wadau wachache muhimu ambao kwa sababu mbalimbali bado hawajafika mbele ya Tume, licha ya kupelekewa mialiko zaidi ya mara moja. 

Taarika hiyo imewataja wadau hao kuwa ni pamoja na baadhi ya viongozi wa dini, viongozi wa baadhi ya vyama vya siasa, taasisi na mashirika yasiyo ya kiserikali na watu binafsi na Wingi wa wananchi wengine wanaoendelea kufika mbele ya Tume kuwasilisha taarifa, ushahidi na ushauri wao. 

Kutokana na fursa hiyo ya Tume kuongezewa muda Tume kupitia Mwenyekiti wake Jaji Othuman Chande inatoa wito kwa wananchi wote kuendelea kuwasilisha ushahidi kwenye Tume kwa kutumia njia zote zilizokuwa zimeainishwa awali ambazo ni majadiliano ya ana kwa ana, mawasilisho ya maandishi (written submissions) kwa njia ya posta au tovuti maalumu ya Tume; barua pepe; ujumbe mfupi wa simu (SMS); kujaza dodoso maalumu kwenye mtandao (www.tume.uchunguzi.go.tz), au kwa kupitia mitandao mingine ya kijamii.

Pia tume hiyo imetoa wito maalumu kwa baadhi ya viongozi wa dini, viongozi wa baadhi ya vyama vya siasa, taasisi na mashirika yasiyo ya kiserikali na watu binafsi ambao wamepewa mialiko na Tume lakini bado hawajafika mbele ya Tume kutumia fursa hii kufika au kuwasiliana na Tume kutoa mchango wao katika uchunguzi unaoendelea kwa manufaa ya wananchi, wadau na nchi kwa ujumla.

Taarifa hiyo pia kupitia Gazeti la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania linaeleza Umma umuhimu wa kuendelea kuipa Tume ushirikiano ili kuiwezesha kukamilisha kazi yake ya uchunguzi. Kama ilivyokuwa mwanzo, Tume itaendelea kufanya vikao vya wazi (public hearing) isipokuwa pale ambapo mashahidi kwa faida ya usalama wao hawapendi majina yao, sura na taarifa zao zitolewe kwenye vyombo vya habari au mitandao ya kijamii. 

Kwa mujibu wa Mpango Kazi, Tume ilipaswa kuwasilisha Taarifa kabla au ifikapo tarehe 20 Februari 2026 ikiwa ndani ya siku 90, ilianza kutekeleza majukumu yake tarehe 20 Novemba, 2025 mara baada ya kuzinduliwa na Mheshimiwa Rais.





Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Mhe. Kheri James, amesema kuwa uongozi wa mkoa umeweka mkakati mahsusi wa kujenga mfumo thabiti na shirikishi wa kuwawezesha vijana kiuchumi, unaojumuisha mafunzo ya ujuzi, upatikanaji wa mitaji pamoja na kuwatafutia masoko ya uhakika kwa bidhaa na huduma zao.

Akizungumza Februari 20, 2026 katika hafla ya ugawaji wa vitendea kazi kwa wajasiriamali iliyofanyika katika Ukumbi wa SIDO, Mhe. Kheri amesema hatua hiyo ni sehemu ya dira ya mkoa kuifanya Iringa kuwa kitovu cha uzalishaji na uongezaji thamani wa rasilimali zilizopo ndani ya mkoa.

Vitendea kazi hivyo vimetolewa kupitia Mradi wa SET (Skills for Employment Tanzania) unaotekelezwa na Swisscontact, ukiwa na lengo la kuwawezesha vijana waliopatiwa mafunzo kuanzisha au kupanua shughuli zao za uzalishaji kwa tija zaidi.

Mhe. Kheri amefafanua kuwa Serikali ya Tanzania chini ya uongozi wa Samia Suluhu Hassan imeendelea kuweka mazingira rafiki yanayochochea ushirikiano kati ya sekta ya umma, sekta binafsi na wadau wa maendeleo, jambo linalorahisisha utekelezaji wa mipango ya kuwainua vijana kiuchumi.

Aidha, amebainisha kuwa mkoa wa Iringa una fursa kubwa kutokana na ardhi yake yenye rutuba kwa shughuli za kilimo, rasilimali za misitu pamoja na sekta ya utalii inayokua kwa kasi, na kusisitiza kuwa rasilimali hizo zikitumika ipasavyo zinaweza kuwa chachu ya ajira na ustawi wa vijana wengi zaidi.








Na Mwandishi WETU, Dodoma

BARAZA la Ardhi na Nyumba la Wilaya, Mkoa wa Dodoma limewasikiliza wananchi wa jamii ya Kiiraqw waliofika katika baraza hilo kuwasilisha hoja na ushahidi wao katika mgogoro wa ardhi, wakidai kumiliki kihalali shamba lenye ukubwa wa ekari nane lililopo Wilaya ya Chamwino, Mkoa wa Dodoma.

Hatua hiyo imekuja kutokana na maombi ya wadaawa hao ambao ni pande mbili zinazohusika katika shauri hilo, kubainisha kuwa wanakabiliwa na changamoto ya lugha, hali iliyokuwa ikiathiri uwezo wao wa kujitetea na kueleza kwa uwazi hoja zao mbele ya Mwenyekiti wa Baraza hilo, Mhe. Omary Mbega.

Kutokana na hilo, Baraza lilitoa huduma ya ukalimani kupitia mkalimani, Simon Tlatlaa Emmay, ambaye alitafsiri maelezo yao na kuwawezesha wadaawa hao kufafanua kwa kina madai yao, kuwasilisha ushahidi pamoja na vielelezo muhimu bila kikwazo cha lugha.

Shauri hilo ni Shauri la Ardhi Na. 92 la mwaka 2025, linalomhusu Ekaristi Ngu’nda kama Mleta Maombi dhidi ya Lolote Nanacha na Martin Lolo Nanacha, ambao ni Wajibu Maombi.

Mgogoro huo unahusu umiliki wa shamba lenye ukubwa wa ekari nane lililopo Kitongoji cha Msunjirire, Kijiji cha Zajilwa, Kata ya Zajilwa, Wilaya ya Chamwino, Mkoa wa Dodoma.

Katika madai yake, Mleta Maombi anadai kuwa ndiye mmiliki halali wa eneo hilo la ardhi, akieleza kuwa ekari hizo ziliuzwa na Wajibu Maombi kwa utaratibu unaozua mgogoro wa kisheria.

Akizungumza mara baada ya kusikilizwa kwa shauri hilo, mmoja wa Wajibu Maombi, Lolo Nanacha, alisema uwepo wa mkalimani umeimarisha imani yake katika mfumo wa utoaji haki.

“Leo nimejisikia huru kueleza ukweli wangu. Nimeeleweka vizuri, na ninaamini haki itatendeka,” alisema.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Baraza hilo Omary Mbega, alisisitiza kuwa huduma ya ukalimani ni sehemu muhimu ya kuhakikisha kila mwananchi anapata haki sawa bila kujali tofauti ya lugha au asili yake.

Shauri hilo limeahirishwa hadi Aprili 15, 2026, ambapo mashahidi zaidi watasikilizwa kabla ya kutolewa uamuzi wa mwisho.



Top News