Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imezindua dawati maalum la uwezeshaji biashara za Forodha kwa wafanyabiashara wa Kariakoo pekee ili kuharakisha upatikanaji wa huduma za kiforodha kwa wafanyabiashara hao.

Akizindua Dawati hilo Februari 10.2026 jijini Dar es Salaam Kamishna Mkuu wa TRA Bw. Yusuph Juma Mwenda amesema uzinduzi wa dawati hilo ni kutekeleza agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan alilolitoa wakati akizindua soko la Kariakoo Februari 08.2026 la kutaka kuwekwa kwa mazingira rahisi ya kufanya biashara.

Amesema lengo la dawati hilo ni kuwezesha na kurahisisha biashara za wafanyabiashara wa Kariakoo ili kuhakikisha biashara zinafanyika kwa urahisi na kwa wakati ikizingatiwa kuwa soko hilo linatoa huduma kwa wafanyabiashara wa ndani na nje ya Tanzania.

Kamishna Mkuu Mwenda amesema dawati hilo maalum litafanya kazi saa 24 na kuwa wanafanya utaratibu wa Bandari kavu nazo zifanye kazi saa 24 na shughuli zitakazofanyika ni kupokea mizigo, kuikagua na kuitoa mapema baada ya taratibu wa ukaguzi kukamilika.

"Niwahakikishie wafanyabiashara wote kuwa TRA imejipanga kuendelea kutenda haki kwa walipakodi wote na kutoa huduma kwa usawa ili kuleta usawa sokoni" amesema Kamishna Mkuu Mwenda.

Kwa upande wake Kamishna wa Forodha na Ushuru wa Bidhaa Bw. Juma Bakari Hassan amesema dawati hilo litaongeza kasi ya utoaji huduma kwa wafanyabiashara wa Kariakoo ambao asilimia kubwa ya mizigo yao inatumia Bandari ya Dar es Salaam.

Kwa upande wao baadhi ya Walipakodi waliokwenda kupatiwa huduma akiwemo Nafsa Momba, Hassan Juma na Richard Haule wamepongeza kuanzishwa kwa dawati hilo ambalo litawqrahisishia kupata huduma za forodha kwa kuwatatulia changamoto ambazo huwa zinajitokeza wakati wa kutoa mizigo.






WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amemwakilisha Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika mkutano wa 43 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Afrika (AUDA-NEPAD) uliofanyika kwa njia ya Mtandao, Ofisini kwa Waziri Mkuu Magogoni Jijini Dar es Salaam.

Akizungumza katika mkutano huo,Dkt. Mwigulu amesema kuwa Tanzania inaendelea kujidhatiti katika kutekeleza Ajenda 2063 kupitia uwekezaji wa kimkakati katika miundombinu, kilimo na maendeleo ya rasilimali watu. 

“Miongoni mwa miradi muhimu ni Mradi wa Umeme wa Maji wa Julius Nyerere, ambao utazalisha megawati 2,115 za umeme pamoja na mradi wa Reli ya Kisasa (SGR) unaounganisha Tanzania na Burundi pamoja na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) ili kuimarisha muunganisho wa kikanda”

Dkt. Mwigulu amesema kuwa Tanzania inaamini kuwa Afrika inaweza kuwa mahali bora zaidi pa kuishi kwa vizazi vya sasa na vijavyo, endapo kila mmoja atajitoa kikamilifu kulinda na kuhifadhi mazingira kwa njia endelevu.

“Ili kufanikisha malengo yetu ya maendeleo ni lazima tuimarishe ukusanyaji wa mapato ya ndani, kupambana na fedha haramu na kutumia ipasavyo utajiri mkubwa wa rasilimali za asili barani Afrika ili kufadhili Ajenda 2063 kwa ufanisi.

Katika mkutano huo  Rais wa Misri Mheshimiwa Abdel Fattah El-Sisi amemaliza muda wake kama mwenyekiti wa Kamati ya Wakuu wa Nchi na Serikali ya AUDA-NEPAD na amekabidhi mamlaka hayo kwa Rais wa Angola, Mheshimiwa João Manuel Gonçalves Lourenço.

Baadhi ya nchi zilizoshiriki mkutano huo ni Misri, Tanzania, Angola, Libya, Afrika Kusini, Ghana, Zimbabwe. Aidha katika mkutano huo, Rais wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) Dkt. Sidi Ould Tah pamoja na Rais na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Afreximbank Dkt. George Elombi walishiriki.




WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amekutana na Kamati ya Kitaifa ya Maandalizi ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON 2027) kwa ajili ya kupitia hatua mbalimbali zilizofikiwa katika maandalizi ya michuano hiyo mikubwa itakayofanyika mwaka 2027 katika nchi za Tanzania, Kenya na Uganda.

Mheshimiwa Dkt. Mwigulu amefanya kikao hicho leo Jumanne (Februari 10, 2026) Ofisi ndogo ya Waziri Mkuu Magogoni jijini Dar es Salaam.

Katika mazungumzo hayo, Waziri Mkuu amepongeza kazi kubwa inayofanywa na kamati hiyo, akieleza kuridhishwa na kasi na mwelekeo wa maandalizi yanayoendelea.

“Maendeleo yaliyofikiwa hadi sasa yanaonesha dhamira ya dhati ya Serikali katika kuhakikisha Tanzania inakuwa mwenyeji bora wa michuano hiyo”.

Waziri Mkuu amesisitiza kuwa ni muhimu kuwepo kwa ushirikishwaji wa sekta zote, “mawaziri, makatibu wakuu pamoja na watendaji wengine hakikisheni mnazishirikisha sekta zetu kila mmoja katika eneo lake, tunataka kuona matokeo chanya katika michuano hii”.

Aidha, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu amewataka wajumbe wa kamati hiyo kuhakikisha kila mmoja anasimamia kikamilifu eneo lake la uwajibikaji, ili hatua zote za maandalizi zikamilike kwa muda uliopangwa na kwa viwango vinavyokubalika.





 

Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) leo, 10 Februari 2026, imetoa msaada wa mashuka 455 katika hospitali ya rufaa ya mkoa wa Iringa ili kuboresha huduma za kimatibabu hospitalini hapo, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa azimio la Baraza la Wafanyakazi wa Mamlaka hiyo, lililofanyika mkoani humo tarehe 9 hadi 10 Februari 2026.

Kaimu Katibu Tawala mkoa wa Iringa, Bi. Nuru Siyovelwa, alipokea msaada huo kwa niaba ya Katibu Tawala Mkoa, na kueleza kuwa, mashuka yamekuwa hayatoshelezi katika hospitali za mkoa huo, hivyo ameishukuru EWURA kwa kuguswa kwani yatasaidia kutoa huduma bora kwa wananchi.

Naye Mganga Mfawidhi wa hospitali hiyo, Dkt. Alfred Mwakalebela, alieleza kuwa mashuka hayo yatapunguza changamoto iliyokuwepo ya upungufu wa mashuka, kwani kwa siku, kila mgonjwa anatakiwa kutumia mashuka 6, ilhali kwa sasa huduma hiyo haitoshelezi kwa kila mgonjwa.

Akiwasilisha msaada huo kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa EWURA, Meneja wa EWURA Kanda ya Kati, Mha. Hawa Lweno, alisema kuwa EWURA itaendelea na utaratibu wa kutoa mchango kwa jamii katika masuala mbalimbali ikiwemo afya.

 


Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi Hesabu Tanzania (NBAA) imeendelea kutoa elimu/mafunzo kwa Vyuo vikuu pamoja na Shule za Sekondari ikiwa na lengo la kuwajengea ufahamu kuhusu shughuli mbalimbali za Bodi na kukuza taaluma ya Uhasibu.

Akizungumza wakati wa kufungua mafunzo hayo Mkurugenzi wa Huduma za Shirika kutoka NBAA CPA Kulwa Malendeja kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa NBAA CPA Pius Maneno amekipongeza chuo hicho kwa kuwa na mwendelezo wa kuwaleta wanachuo wanaosoma masomo ya Uhasibu na Biashara kwenye Bodi hiyo ili kupata elimu kuhusu kazi mbalimbali zinazofanywa na Bodi.

Malendeja amesema ili kuwa Mhasibu au Mkaguzi inabidi kufanya mitihani ya Bodi hiyo ili kupewa cheti cha kitaaluma ili uweze kutambulika kisheria kama Mhasibu au Mkaguzi ambapo cheti hicho kitakutambulisha kitaifa na kimataifa na kuweza kufanya kazi nje na ndani ya nchi.

"Nimefarijika kuona wanafunzi wa Sheria pia  wakishiriki katika ziara hii na kupata mafunzo kwani wana nafasi ya kusomea masomo ya Uhasibu na kuwa CPA yaani "Certified Public Accountant" alisema Malendeja

Naye Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na Mawasiliano wa NBAA, Magreth Kageya amesema ziara hiyo imekuwa chachu kwa wanafunzi kwani wanapata taarifa mbalimbali kuhusu NBAA

Aliongeza kuwa kupitia matukio  mbalimbali NBAA husikiliza maoni na mapendekezo mbalimbali kuhusu huduma zake kwa mfano NBAA imesikia kilio cha wadau wake kuhusu ucheleweshwaji wa vyeti vya Kitaaluma kwa kuomba Bodi kusaidia upatikanaji wa vyeti mapema wanapomaliza na sio kwa kusubiri kwa muda mrefu. Na sasa NBAA imeamua kuanzisha Mahafali nyingine ili kukidhi mahitaji ya wadau wake, na kwa mara ya kwanza mahafali hayo yatafanyika tarehe 28 Machi, 2026 katika ukumbi wa APC Bunju jijini Dar es Salaam. Maana yake kwa mwaka kutakuwa na mahafali mbili yaani Machi na Septemba au Oktoba mwanzoni.

Naye mwalimu wa Chuo Kikuu cha Kiislamu cha Morogoro Dkt. Ayubu Timba ameishukuru NBAA kwa mwaliko wa wanafunzi kuja kupata Elimu ya Uhasibu.

Aliongeza kuwa wanachuo hao waliotembelea na kupata elimu ya Uhasibu itawapa dira na mwelekeo mzuri sasa na hapo baadae na pia aliwasisitiza wanachuo hao kwenda kuwa mabalozi kwa wenzao na jamii kwa ujumla.

Baadhi ya Wafanyakazi wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA) wakiwa kwenye picha ya pamoja na Wanachuo wa Chuo Kikuu cha Kiislamu cha Morogoro wanaosoma masomo ya Uhasibu mara baada ya kumaliza mafunzo yaliyofanyika katika ofisi za Bodi hiyo jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi wa Huduma za Shirika kutoka NBAA CPA Kulwa Malendeja akitoa salamu za Bodi kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu (NBAA), CPA Pius A. Maneno wakati wa ziara ya masomo ya wanachuo wa Chuo Kikuu cha Kiislamu cha Morogoro waliotembelea Bodi hiyo kwa ajili ya kujifunza mambo mbalimbali ya Bodi.
Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na Mawasiliano wa NBAA, Magreth Kageya akitoa mada kuhusu kazi mbalimbali zinazofanywa na NBAA "NBAA Overview"  kwa wanachuo wa Chuo Kikuu cha Kiislamu cha Morogoro waliotembelea Bodi hiyo kwa ajili ya kujifunza mambo mbalimbali ya Bodi.
CPA Esther Masalla akiwasilisha mada kuhusu uanachama, jinsi ya kupanda daraja na usajili wa makampuni ya kihasibu na kikaguzi wakati wa ziara ya wanachuo wa Chuo Kikuu cha Kiislamu cha Morogoro.
CPA Praygod Munuo akitoa mada kuhusu misingi ya fedha kwa wanachuo wa Chuo Kikuu cha Kiislamu cha Morogoro
Rebecca Siame akizungumzia usajili, madaraja mbalimbali ya mitihani ya Taaluma ya Uhasibu na jinsi ya kufanya mitihani hiyo kwa wanachuo wa Chuo Kikuu cha Kiislamu cha Morogoro
Rais wa  wanafunzi wanaosoma masomo ya Uhasibu katika Chuo Kikuu cha Kiislamu cha Morogoro (MUMASO)  Benjamin Mussa akitoa neno la shukrani kwa uongozi wa NBAA kufuatia kufanikishwa kwa ziara yao katika ofisi hiyo
Baadhi ya wanachuo wa Chuo Kikuu cha Kiislamu cha Morogoro wakichangia mada pamoja na kuuliza maswali kwa watoa mada mbalimbali wakati wa ziara yao ofisi za NBAA jijini Dar es Salaam.
Baadhi ya wanachuo wanaosoma masomo ya Uhasibu kutoka Chuo Kikuu cha Kiislamu cha Morogoro wakifuatilia mada mbalimbali zilizokuwa zinatolewa na wataalamu kutoka NBAA.
Mwalimu wa Chuo Kikuu cha Kiislamu cha Morogoro Dkt. Ayubu Timba akitoa neno la shukrani kwa NBAA kwa niaba ya uongozi wa chuo hicho.

Top News