ZAIDI ya wananchi 8,000 kutoka Mkoa wa Arusha na maeneo mengine nchini wamepata huduma za uchunguzi na matibabu bila malipo katika siku mbili za kwanza za kambi maalumu ya afya inayofanyika jijini Arusha. Kambi hiyo ya siku saba ilianza Julai 13, 2026 na itahitimishwa Julai 19, ambapo wananchi wanapatiwa vipimo, ushauri wa madaktari bingwa, matibabu, dawa na rufaa bila malipo.
Kambi hiyo imeandaliwa na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Arusha kwa kushirikiana na Ofisi ya Mbunge wa Arusha Mjini, Paul Makonda, pamoja na Wizara ya Afya, hospitali za rufaa za kitaifa, taasisi maalumu za afya na hospitali binafsi. Katika siku ya kwanza wananchi 3,500 walihudumiwa, huku zaidi ya 4,500 wakipata huduma siku ya pili na kufanya jumla ya walionufaika kufikia zaidi ya 8,000.
Huduma zinazotolewa ni pamoja na vipimo mbalimbali vya afya, ushauri wa kitaalamu, matibabu, dawa na rufaa. Aidha, zaidi ya watu 50 walijitokeza kuchangia damu katika banda la Mpango wa Taifa wa Damu Salama, huku wagonjwa waliobainika kuhitaji matibabu ya kina wakipelekwa hospitalini kwa magari ya wagonjwa.
Akizungumza katika kambi hiyo, Makonda alimshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, Wizara ya Afya, madaktari, taasisi za afya na sekta binafsi kwa kuwezesha huduma za kibingwa kuwafikia wananchi wa Arusha na maeneo ya jirani. Alisema mafanikio hayo yametokana na ushirikiano mzuri kati ya Serikali, viongozi wa wananchi, hospitali za rufaa na wadau wa sekta ya afya.
Makonda alisema wananchi wengi wanaofika kambini hawana uwezo wa kumudu gharama za vipimo na matibabu katika mazingira ya kawaida, huku baadhi wakishindwa kuendelea na matibabu baada ya fedha zao kuishia kwenye vipimo vya awali.
Alieleza kuwa ingawa wananchi wanapata huduma hizo bila malipo, taasisi, hospitali, madaktari na wadau wameingia gharama kubwa za usafiri, vifaa vya uchunguzi, dawa, miwani, malazi, chakula na mahitaji mengine muhimu ili kuhakikisha huduma zinawafikia wananchi.
Aliwasihi wananchi wanaopewa dawa, miwani na maelekezo ya matibabu kuyafuata kikamilifu, akisisitiza kuwa dawa na huduma zote zilizotolewa zimegharimiwa na hivyo ni muhimu zitumike ipasavyo ili kuleta matokeo yaliyokusudiwa.
Pia aliwahimiza wafanyabiashara, wamachinga, waendesha bodaboda na bajaji pamoja na wananchi wengine kutenga muda wa kupima afya, akisisitiza kuwa huduma hizo zinapatikana kwa watu wote bila kujali wanakotoka, dini, kabila, chama cha siasa au hali yao ya kiuchumi.