Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

WAKALA wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) umesema usimamizi endelevu wa misitu na rasilimali za nyuki ni nguzo muhimu katika kuimarisha usalama wa mazingira, kukuza uchumi na kujenga jamii zenye ustahimilivu dhidi ya athari za mabadiliko ya tabianchi barani Afrika.

Kauli hiyo imetolewa Julai 21,2026 wakati TFS ikishiriki katika Kongamano la Pili la Wahitimu wa Chuo cha Taifa cha Ulinzi Tanzania, linalowakutanisha viongozi, wataalamu na wadau mbalimbali kujadili mwenendo wa siasa, uongozi, uchumi na usalama duniani pamoja na athari zake kwa maendeleo ya Afrika.

Akizungumza kwa niaba ya Kamishna wa Uhifadhi wa TFS, Prof. Dos Santos Silayo, Mhifadhi Mkuu wa TFS, PCO. Kassim Ally, alisema sekta ya misitu na nyuki imevuka dhana ya kuwa ya uhifadhi wa mazingira pekee na sasa ni mhimili muhimu wa uchumi, usalama wa jamii na maendeleo endelevu.

Alisema misitu inalinda vyanzo vya maji, huhifadhi bioanuwai, husaidia kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi, huzalisha ajira na kuongeza kipato cha wananchi kupitia matumizi endelevu ya rasilimali zake.

“Misitu si chanzo cha mbao pekee, bali ni msingi wa ustawi wa jamii kwa kulinda vyanzo vya maji, kuhifadhi bioanuwai, kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi, kutoa ajira na kuongeza kipato kwa wananchi kupitia shughuli mbalimbali zinazotegemea rasilimali za misitu,” alisema PCO. Kassim.

Aliongeza kuwa rasilimali za misitu na nyuki zina mchango mkubwa katika kuimarisha usalama wa taifa kupitia uhakika wa chakula, maji, nishati, afya na fursa za kiuchumi zinazojenga jamii imara na zinazostahimili changamoto mbalimbali.

Katika maonesho ya kongamano hilo, TFS ilitoa elimu kuhusu fursa zinazotokana na matumizi endelevu ya misitu na nyuki, ikiwemo ufugaji wa nyuki, uzalishaji wa bidhaa zenye thamani iliyoongezwa kama Honey Nuts na Stingless Honey Garlic, ambazo zimeendelea kuvutia wadau kutokana na ubunifu wake na uwezo wa kuongeza kipato kwa wananchi.

Huduma ya tiba kwa kutumia mazao ya nyuki (Apitherapy), hususan tiba ya kudungwa na nyuki, nayo ilikuwa miongoni mwa vivutio vikubwa katika banda la TFS, huku washiriki wakipata elimu kuhusu matumizi ya mazao ya nyuki katika kuboresha afya na ustawi wa jamii.

Mbali na hilo, TFS ilitumia kongamano hilo kutangaza fursa za utalii ikolojia zinazopatikana katika misitu ya hifadhi nchini, ikieleza kuwa utalii huo umeendelea kuchangia mapato ya taifa, ajira na uwekezaji sambamba na kuhamasisha uhifadhi wa rasilimali za misitu.

Kongamano hilo, lenye kaulimbiu isemayo “Mwenendo wa Siasa, Uongozi, Uchumi na Usalama Duniani katika Karne ya 21 na Athari zake kwa Maendeleo ya Afrika,” limeweka bayana umuhimu wa sekta mbalimbali kushirikiana katika kujenga uchumi imara na usalama wa bara la Afrika.

TFS imesema ushiriki wake katika kongamano hilo unaendana na jitihada za Serikali za kuhakikisha rasilimali za misitu na nyuki zinatumika kama kichocheo cha maendeleo ya taifa kupitia uhifadhi wa mazingira, ukuaji wa uchumi, ajira na ustahimilivu wa jamii dhidi ya athari za mabadiliko ya tabianchi.

Kwa mujibu wa PCO Kassim, usimamizi madhubuti wa misitu na nyuki umeendelea kuwa nyenzo muhimu ya kujenga usalama wa mazingira, kuimarisha uchumi wa wananchi na kuchochea maendeleo endelevu ya Tanzania na Afrika katika karne ya 21.











Katika uongozi ni uwekezaji katika uchumi wa Taifa. Kadiri tunavyojenga viongozi wenye uwezo, ndivyo tunavyojenga taasisi zenye tija na kuongeza mchango wake katika mapato ya Serikali,” alisema.

Alisema katika kipindi cha utekelezaji wa DIRA 2050, Ofisi ya Msajili wa Hazina imeainisha maeneo matano ya kimkakati yatakayoongoza mageuzi ya Taasisi za Umma.

Maeneo hayo ni kuimarisha utawala bora, kuendeleza uongozi na rasilimali watu, kuimarisha usimamizi wa utendaji unaotegemea viashiria na ushahidi, kuwezesha upatikanaji wa rasilimali kupitia ubia kati ya sekta ya umma na binafsi (PPP), masoko ya mitaji na mifuko ya uwekezaji, pamoja na kuongeza tija, faida na thamani ya uwekezaji wa Serikali.

Aliongeza kuwa mafanikio ya maeneo hayo yanategemea pia ushirikiano wa karibu kati ya Taasisi za Umma na sekta binafsi, ili kuongeza uwekezaji, matumizi ya teknolojia, ubunifu, ushindani wa uchumi na ajira.

Naye Bw. Kadari Singo, Afisa Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Uongozi, alisema kuwa mafanikio ya utekelezaji wa Dira 2050 yatategemea kwa kiasi kikubwa uwepo wa mfumo imara wa uongozi.

Alisema ni muhimu kujenga mifumo ya kutambua na kuendeleza vipaji vya uongozi, kuhakikisha viongozi wanawekwa katika nafasi zinazolingana na uwezo wao, kuweka mipaka ya wazi ya mamlaka na majukumu yao, pamoja na kuimarisha uwajibikaji katika ngazi zote za uongozi.

"Masuala haya yanapaswa kupewa kipaumbele na kuzingatiwa kikamilifu katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050," alisema.

Katika mafunzo hayo ya siku nne, washiriki watapata mada kuhusu afya na ustawi wa viongozi, kufungamanisha mipango ya taasisi na DIRA 2050, uongozi wa kimkakati, usimamizi wa migogoro, usimamizi wa uwekezaji wa Serikali, utawala bora, usimamizi wa vihatarishi, ESG, fedha, ukaguzi pamoja na zoezi la kuandaa ahadi binafsi za utekelezaji wa DIRA 2050.





SERIKALI imesema hakuna tena biashara ya kawaida kwa Taasisi, Mashirika ya Umma na Wakala za Serikali. Waziri Prof. Kitila Mkumbo amesema viongozi lazima wafanye kazi kwa kuzingatia matokeo, ubunifu na uwajibikaji ili kuharakisha Dira ya Taifa 2050.

Akizungumza Kibaha wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya viongozi 57, Prof. Mkumbo amesema lengo la Taifa ni kufikia uchumi wa dola Trilioni 1 ifikapo 2050. Amesema hilo litafanikiwa kama viongozi watatafsiri maono hayo kuwa huduma na miradi inayoonekana kwa wananchi.

Waziri amesisitiza kuwa mafanikio hayatapimwa kwa vikao bali kwa tija, uwekezaji na ajira. Pia amewataka viongozi kushirikiana na sekta binafsi kwani ndio injini ya ukuaji wa uchumi. "Tuache kuwa vikwazo kwa wawekezaji" amesema.

Msajili wa Hazina Bw. Nehemiah Mchechu amesema tangu 2024 viongozi 187 wameshafundishwa. Matokeo yake makusanyo ya gawio yameongezeka kutoka Sh bilioni 637 hadi Sh Trilioni 1.3. Ofisi yake imeweka vipaumbele 5 vya mageuzi ikiwemo utawala bora na ubia wa umma na binafsi

Katika mafunzo ya siku 4, viongozi watapata mafunzo ya uongozi wa kimkakati, usimamizi wa uwekezaji na utawala bora.






Na Mwandishi Wetu,Korea
TANZANIA imeendelea kuonesha uwezo wake katika jukwaa la kimataifa la UNESCO baada ya Bi. Rose Kinabo kuiwakilisha nchi katika Jukwaa la Vijana Wataalamu wa Urithi wa Dunia 2026, linalofanyika sambamba na Kikao cha 48 cha Kamati ya Urithi wa Dunia jijini Busan, Jamhuri ya Korea.

Katika kuonesha kutambua mchango huo, Balozi na Mwakilishi wa Kudumu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika UNESCO, Mheshimiwa Saidi Yakubu, amekutana na Bi. Kinabo na kumpongeza kwa kuiwakilisha Tanzania kwa weledi na umahiri, baada ya kuchaguliwa kupitia mchakato wa ushindani mkubwa uliowashirikisha vijana kutoka mataifa 29 duniani.

Mheshimiwa Balozi Yakubu alisema mafanikio hayo yanaendelea kuthibitisha kuwa Tanzania ina hazina ya wataalamu vijana wenye uwezo wa kushiriki na kuchangia mijadala ya kimataifa kuhusu uhifadhi, usimamizi na maendeleo endelevu ya Urithi wa Dunia.

Bi. Kinabo, ambaye ni Mhadhiri Msaidizi katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na mtaalamu wa usimamizi wa urithi kwa kushirikisha jamii, aliwasilisha uzoefu wa Tanzania kuhusu usimamizi shirikishi wa maeneo ya Urithi wa Dunia pamoja na mchango wa taasisi za elimu katika kulinda na kuendeleza urithi huo. Uwasilishaji wake uliendana na kaulimbiu ya jukwaa la mwaka huu isemayo, “World Heritage, Communities and Education: Empowering Youth as Agents of Change.”

Mheshimiwa Balozi Yakubu alibainisha kuwa ushiriki wa Tanzania katika majukwaa ya vijana ya UNESCO unaimarisha sauti ya taifa katika masuala ya urithi wa dunia na kufungua fursa mpya za ushirikiano wa kitaalamu, utafiti, ubunifu na kujengeana uwezo kati ya wataalamu wa Tanzania na wenzao kutoka mataifa mbalimbali.

Aidha, alisisitiza kuwa Serikali itaendelea kuwekeza katika kuwawezesha vijana kushiriki kikamilifu katika majukwaa ya kimataifa, akieleza kuwa vijana ni nguvu muhimu katika kulinda urithi wa dunia na kuendeleza ajenda ya maendeleo endelevu kupitia elimu, utamaduni na ubunifu.

Katika kikao hicho, Mheshimiwa Balozi Yakubu aliambatana na Katibu Mtendaji wa Kamisheni ya Taifa ya UNESCO Tanzania, Profesa Hamisi Malebo, pamoja na maafisa wengine waandamizi wa ujumbe wa Serikali ya Tanzania unaoshiriki Kikao cha 48 cha Kamati ya Urithi wa Dunia.

Ushiriki wa Bi. Rose Kinabo umechangia katika maandalizi ya Azimio la Vijana la UNESCO kuhusu Urithi wa Dunia, litakalowasilishwa rasmi mbele ya Kamati ya Urithi wa Dunia. Mafanikio hayo yanaendelea kuitangaza Tanzania kama nchi inayowekeza katika vijana, maarifa na ushirikishwaji wa jamii kama nguzo muhimu za kulinda na kuendeleza Urithi wa Dunia kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.



Na Oscar Assenga, Tanga

Mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Salum Nyamwese, amewataka wakurugenzi wa halmashauri kuhakikisha kila fedha inayotolewa na Serikali kwa ajili ya miradi ya maendeleo inasimamiwa kwa uadilifu na kutumika kulingana na malengo yaliyokusudiwa.

Nyamwese ambaye ni Mkuu wa Wilaya ya Handeni amesema matumizi mabaya ya fedha za umma, rushwa na ubadhirifu vinaweza kuwa kikwazo kikubwa katika kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2050.

Alitoa kauli hiyo mjini Tanga wakati akifungua warsha ya wadau wa usimamizi na utekelezaji wa miradi ya maendeleo mkoa wa Tanga iliyoandaliwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), iliyowakutanisha wakurugenzi wa halmashauri, wakuu wa taasisi za umma na viongozi mbalimbali kwa ajili ya kujadili namna ya kuimarisha uwajibikaji na usimamizi wa rasilimali za umma.

Nyamwese alisema fedha zinazotolewa na Serikali ni mali ya wananchi, hivyo viongozi wenye dhamana wanapaswa kuhakikisha kila shilingi inatumika kwa ufanisi na kuleta manufaa yaliyokusudiwa.

“Fedha zinazotolewa na Serikali ni mali ya wananchi hivyo ni wajibu wa kila mkurugenzi kuhakikisha hakuna hata shilingi moja inayopotea au kutumika nje ya malengo yaliyokusudiwa. Tunapaswa kusimamia miradi kwa uadilifu na kuhakikisha wananchi wanaona thamani ya fedha zinazotolewa,” alisema.

Alisema warsha hiyo imefanyika wakati muafaka ambapo Serikali imeanza utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayolenga kujenga uchumi shindani, taasisi imara, uwajibikaji na matumizi yenye tija ya rasilimali za umma.

Kwa mujibu wa Nyamwese, utekelezaji wa dira hiyo hauwezi kufanikiwa iwapo viongozi hawataweka mbele maslahi ya wananchi na kupambana kikamilifu na vitendo vya rushwa, ubadhirifu na ukiukwaji wa taratibu.

“Rushwa ni adui mkubwa wa maendeleo kwani huhujumu matumizi sahihi ya rasilimali za umma, hudhoofisha utekelezaji wa miradi ya maendeleo, hupunguza ubora wa huduma zinazotolewa kwa wananchi na kuondoa imani ya wananchi kwa taasisi za Serikali,” alisema.

Aliwataka wakurugenzi kushirikiana kwa karibu na Takukuru katika kuimarisha mifumo ya udhibiti wa ndani, kuongeza uwazi katika matumizi ya fedha za umma na kuchukua hatua mapema dhidi ya viashiria vya ubadhirifu.

Nyamwese alisema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuelekeza uwekezaji mkubwa katika Mkoa wa Tanga kwa lengo la kuboresha huduma za kijamii na kuchochea ukuaji wa uchumi.

Alieleza kuwa katika kipindi cha miaka mitano kuanzia mwaka wa fedha 2021/2022 hadi 2025/2026, Mkoa wa Tanga umepokea zaidi ya Sh trilioni 3 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali katika sekta za elimu, afya, maji, kilimo, mifugo, uvuvi, biashara, uwekezaji, miundombinu ya barabara, nishati, ardhi na uwezeshaji wananchi kiuchumi.

Hata hivyo, alisema kiasi hicho kikubwa cha fedha hakitakuwa na maana bila kuwepo kwa usimamizi mzuri, ufuatiliaji wa karibu na uwajibikaji wa viongozi wanaosimamia miradi hiyo.



“Fedha pekee hazileti maendeleo. Kinacholeta maendeleo ni usimamizi mzuri, ufuatiliaji wa karibu na uwajibikaji wa viongozi wanaosimamia utekelezaji wa miradi,” alisisitiza.

Aliwataka wakurugenzi kufanya tathmini za mara kwa mara za miradi inayotekelezwa katika maeneo yao, kuhakikisha kazi zinafanyika kwa viwango vinavyotakiwa na kuchukua hatua dhidi ya watumishi au wakandarasi watakaobainika kukiuka sheria.

Akizungumzia fursa za maendeleo zilizopo mkoani Tanga, Nyamwese alisema mkoa huo unatarajiwa kuwa kitovu kikubwa cha biashara na uwekezaji kutokana na utekelezaji wa miradi ya kimkakati, ikiwemo uboreshaji wa Bandari ya Tanga, reli ya kisasa (SGR) pamoja na Mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP).


Alisema miradi hiyo itaongeza shughuli za kiuchumi na kuvutia wawekezaji wengi zaidi, hivyo viongozi wa halmashauri wanapaswa kuhakikisha mazingira ya uwazi, uwajibikaji na matumizi sahihi ya rasilimali yanaendelea kuimarishwa.

Awali, akizungumza katika warsha hiyo, Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa ( TAKUKURU) Ramadhan Ndwatah alisema taasisi hiyo imefanya tathmini ya miradi inayotekelezwa ndani ya Mkoa wa Tanga na kubaini baadhi ya changamoto zinazotokana na usimamizi usioridhisha.

Alisema changamoto hizo ni pamoja na ucheleweshwaji wa miradi, matumizi yasiyo sahihi ya fedha, ongezeko la gharama zisizo za lazima na kupungua kwa manufaa yaliyotarajiwa kwa wananchi.

“Licha ya mafanikio yaliyopatikana kwenye miradi ya maendeleo, bado kuna changamoto ya udhaifu katika utekelezaji wa miradi, ucheleweshwaji wa miradi kwabaadhi ya wadau wenye dhamana, kuongeza gharama zisizo za lazima na kupunguza manufaa yanayotarajiwa kwa wananchi,” alisema.

Alisema kutokana na changamoto hizo, wameona ni muhimu kukutana na wadau wa usimamizi na utekelezaji wa miradi ili kuwakumbusha wajibu wao katika kuhakikisha miradi inatekelezwa kwa ufanisi.

Aliwataka wadau wote wenye dhamana ya kusimamia miradi kushirikiana na TAKUKURU ili kutimiza azma ya Serikali ya kuwaletea wananchi maendeleo kupitia miradi mbalimbali.


Mkurugenzi Tanga Jiji atoa ushauri kuhusu BOQ

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Tanga, Mhandisi Juma Hamsini, aliiomba Serikali kupitia Ofisi ya Rais – TAMISEMI kuzingatia thamani halisi ya vifaa vinavyotumika wakati wa kuandaa BOQ za miradi mbalimbali ya ujenzi, ikiwemo madarasa.

Alisema hatua hiyo itasaidia kuhakikisha gharama zinazowekwa kwenye miradi zinaendana na hali halisi ya soko na kusaidia utekelezaji wa miradi yenye ubora na thamani kwa wananchi.




NMB Bank Plc has advanced its Medium-Term Plan 2026–2030, (Agenda 2030), by committing approximately USD 100 million (TZS 224 billion) to a landmark USD 500 million syndicated financing facility arranged by Nedbank Corporate and Investment Banking for AngloGold Ashanti's Geita Gold Mine.

The commitment makes NMB the largest Tanzanian bank participating in the transaction, highlighting its growing capacity to mobilise domestic capital for strategic investments that support national development while reinforcing its position as a leading financier of Tanzania's productive sectors.

The financing aligns with NMB's Agenda 2030 strategy, which identifies mining as a key driver of economic growth. By supporting one of Tanzania's largest mining operations, the bank is helping strengthen foreign exchange earnings, local value chains, employment and the country's industrial and export competitiveness.

The investment also supports the ambitions of Tanzania Development Vision 2050 by promoting private-sector-led growth, industrialisation, export expansion and greater local participation in strategic industries.

As one of Tanzania's flagship mining operations and among Africa's leading gold producers, Geita Gold Mine is a major contributor to the national economy. The facility will support AngloGold Ashanti's continued investment in the mine, sustaining production, exports, local procurement, jobs and long-term economic value.

Commenting on the milestone, NMB Bank Plc Managing Director and Chief Executive Officer, Ruth Zaipuna, said the transaction reflects the bank's strategy of directing capital toward sectors with the greatest potential to transform Tanzania's economy.

"This transaction demonstrates NMB's ability to participate in sophisticated, large-scale financing alongside leading regional and international financial institutions while ensuring Tanzanian capital plays a meaningful role in financing nationally strategic investments. It is Agenda 2030 in action, deploying our balance sheet, expertise and partnerships to accelerate sustainable economic growth and long-term national prosperity."

She added:

"Tanzania Development Vision 2050 sets out an ambitious pathway towards a more competitive, inclusive and industrialised economy. Financing investments of this scale enables us to strengthen a sector that drives exports, foreign exchange earnings, local enterprise development, employment and sustainable economic transformation."

NMB's participation further reinforces its role as a long-term financial partner to Tanzania's mining industry. To date, the bank has cumulatively financed the sector with approximately TZS 400 billion, supporting responsible mining, local supplier development and investment across the mining value chain.

The Geita financing also demonstrates the growing ability of African financial institutions to collaborate on complex transactions that mobilise long-term capital for strategic investments across the continent.

NMB Bank commended Nedbank Corporate and Investment Banking for arranging and underwriting the syndicated facility, noting that the transaction reflects the strength of regional financial partnerships in advancing Africa's sustainable economic development.



Balozi wa Tanzania nchini Algeria, Mhe Mobhare Matinyi, akizungumza na vyombo vya habari vya Algeria wakati akitangaza kuwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imekubali mwaliko wa kuwa mgeni rasmi katika Maonesho ya Ufugaji wa Nyuki barani Afrika (Africa Bee Expo) yatakayofunguliwa jijini Algiers mnamo Septemba 3, 2026.
Bw. Fatah Benchouia, Mwenyekiti wa Maonesho ya Ufugaji wa Nyuki barani Afrika (Africa Bee Expo) ya mwaka 2026, akizungumza na vyombo vya habari vya Algeria wakati wa kuitangaza Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa mgeni rasmi.

TANZANIA imekubali mwaliko wa kuwa mgeni rasmi katika ufunguzi wa Maonesho ya Ufugaji wa Nyuki barani Afrika yatakayofanyika jijini Algiers, Algeria, tarehe 3-6 Septemba, 2026.


Akizunngumza na waandishi wa habari wa televisheni za Algeria kwenye Ubalozi wa Tanzania jijini Algiers, Balozi Mobhare Matinyi alisema Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji, ndiye atakayefungua maonesho hayo kwa niaba ya serikali.


Balozi Matinyi alisema Mhe. Waziri Dkt. Kijaji atakuja Algeria akiongoza ujumbe wa maafisa waandamizi na wataalamu wa serikali pamoja na wadau kutoka sekta binafsi ya ufugaji wa nyuki na utengenezaji wa bidhaa za nyuki nchini.


Balozi Matinyi alisema serikali inaipa sekta ya ufugaji wa nyuki umuhimu wa kipekee kwani inaajiri watu wapatao milioni mbili nchini na huingiza dola za Marekani milioni 77.5 (shilingi bilioni 205) kwa mwaka kutokana na mauzo ya asali katika nchi mbalimbali duniani.


Akinukuu takwimu za serikali, Balozi Matinyi alisema Tanzania hivi sasa ni ya pili kwa uzalishaji asali barani Afrika na ya kumi duniani na bado ikijipanga zaidi ina uwezo wa kufikisha mizinga ya nyuki takribani milioni 9.2 yenye uwezo wa kuzalisha tani 138,000 za asali na tani 9,200 za nta kwa mwaka.


Awali Mwenyekiti wa taasisi ya Algeria inayoandaa maonesho hayo, Fatah Benchouia, aliwaambia waandishi wa habari kwamba mbali ya uhusiano mzuri uliopo baina ya Algeria na Tanzania, lakini pia sababu kuu ya kuipa Tanzania heshima hii ni mafanikio yake katika sekta ya ufugaji wa nyuki ambapo kwa mwaka huzalisha tani 34,000 za asali kulinganisha na Algeria inayozalisha tani 7,300.


Bw. Benchouia aliambatana na Mwenyekiti wa Baraza la Kisayansi la taasisi inayoandaa maonesho hayo, Dkt. Abdelmadjid Bouchareb, pamoja na Rais na Afisa Mtendaji Mkuu wa Kituo cha Biashara cha Dunia hapa Algeria, Bw. Ahmed Tibaoaoui.


Maonesho hayo maarufu kwa jina la Africa Bee Expo 2026, yanafanyika kwa mara ya nne hapa Algeria na Tanzania inatarajia kuonesha mafanikio yake katika sekta hii na kujifunza kutoka kwa wafugaji na wazalishaji wa bidhaa za nyuki wa nchi zingine.


Imetolewa na Ubalozi wa Tanzania,
Algiers, Julai 20, 2026.

Katika kuhakikisha Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya linatoa huduma bora kwa wananchi kwa kutumia vifaa vya kielektroniki pamoja na mifumo mbalimbali ya kidigitali, wananchi na wadau Mkoani humo wapongezwa kwa kuendelea kushirikiana na Jeshi hilo katika kuzuia na kutokomeza uhalifu.

Hayo yamesemwa na Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Wilbert Siwa Julai 21, 2026 wakati akipokea msaada wa "Computer" iliyotolewa na Diwani wa Kata ya Ilemi kwa ajili ya kusaidia kazi za Polisi Jamii Wilaya ya Mbeya.

"Msaada huu umekuja wakati muafaka ambapo Jeshi la Polisi nchini limejikita katika matumizi ya mifumo mbalimbali ya kidigitali katika utendaji wake wa kazi, hivyo vifaa hivi vitasaidia kuongeza ufanisi na weledi katika utekelezaji wa majukumu mbalimbali" alisema Kaimu Kamanda Siwa.

Aidha, Kaimu Kamanda Siwa amesema kuwa elimu inayotolewa na Polisi na Wakaguzi Kata kwa makundi mbalimbali imesaidia wananchi kujua wajibu wao na kuzaa matunda ikiwemo kupungua kwa matukio ya uhalifu na kupata misaada mbalimbali ya vitendea kazi kama hivi vilivyotolewa na Waheshimiwa Madiwani wa Halmashauri ya Jiji la Mbeya.

Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Ilemi Mhe Baraka Zambi amesema kuwa, msaada huo umetolewa kutokana na ushirikiano mzuri uliopo kati ya Jeshi la Polisi na Wananchi katika maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Mbeya.

Aidha, Mhe Zambi amesema kuwa, kutokana na uwepo wa Polisi Jamii kwa sasa katika Kata ya Ilemi uhalifu umepungua ukilinganisha na hapo awali, vijana wameelimishwa na kubadilika na kubadili mienendo yao.

Naye, Diwani wa Kata ya Iwambi Mhe Gloria Mwamajemba maarufu Mchina amesema kuwa Polisi Kata wameleta matokeo chanya katika kuimarisha ulinzi na usalama kutokana na elimu inayotolewa pamoja na ushirikiano mkubwa uliopo kati ya Jeshi la Polisi na wananchi.

Kupitia falsafa ya Polisi Jamii, Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya limeendelea kushirikiana na wananchi kupitia utekelezaji wa miradi mbalimbali ya Polisi Jamii na kupelekea kupata mafanikio chanya ikiwemo kupungua kwa uhalifu.








TANZANIA inalenga kuongeza ushiriki wake katika soko la kimataifa la kaboni, huku kituo cha Taifa cha Ufuatiliaji wa Kaboni (NCMC) kikipewa jukumu la kuimarisha usimamizi, kuvutia uwekezaji wa kijani na kuongeza manufaa ya rasilimali za asili.

Katibu Mkuu katika Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Richard Muyungi, amesema Tanzania inapaswa kubadilika kutoka kuwa mshiriki wa kawaida katika biashara ya kaboni na kuwa miongoni mwa nchi zinazoongoza kwa kujenga mifumo thabiti itakayowezesha utekelezaji wa miradi ya kaboni yenye uadilifu wa hali ya juu.

Katibu Huyo Mkuu amesema hayo Julai 21 2016 jijini Dar es Salaam kwenye kikao  cha kwanza cha Bodi ya Wakurugenzi ya Kituo Cha Kaboni nchini kwa mwaka wa fedha 2026/2027.

Dkt. Muyungi amesema ukuaji wa uchumi wa kaboni duniani ni fursa muhimu kwa Tanzania kuongeza mapato ya Taifa sambamba na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

“Changamoto yetu sasa siyo kushiriki tu katika masoko ya kaboni, bali kuyaongoza,” alisema Dkt. Muyungi.

Amesema soko la kaboni duniani linaendelea kukua kwa kasi na sasa linakadiriwa kuwa na thamani ya zaidi ya dola za Marekani bilioni 107 kwa mwaka, huku Afrika ikiwa na uwezo wa kuzalisha takribani dola bilioni 6 kwa mwaka ifikapo 2030 endapo itatumia kikamilifu fursa zilizopo.

Dkt. Muyungi amesema Tanzania ina nafasi kubwa ya kunufaika kutokana na utajiri wa rasilimali zake ikiwemo misitu, maeneo oevu, mifumo ya ikolojia ya pwani na bahari, pamoja na fursa zilizopo katika nishati safi na kilimo kinachozingatia mabadiliko ya tabianchi.

Ameeleza kuwa hadi sasa Tanzania imesajili miradi 99 ya kaboni, huku zaidi ya mikopo ya kaboni milioni 13.4 ikiwa imetolewa. Hata hivyo, amesema mafanikio hayo bado hayajaakisi thamani halisi ya kiuchumi inayoweza kupatikana kupitia sekta hiyo.

“Mafanikio haya hayaoneshi manufaa yote tunayotarajia kutoka kwenye sekta ya kaboni. Tunahitaji kufanya zaidi kuhakikisha miradi inafikia hatua ya utekelezaji na kuanza kuleta thamani kwa Taifa na jamii zetu,” alisema.

Kutokana na hali hiyo, Dkt. Muyungi aliitaka bodi ya Kituo hicho kuimarisha mifumo ya usajili wa miradi ya kaboni, kuharakisha utekelezaji wa mifumo ya Ibara ya 6 ya Mkataba wa Paris kuhusu biashara ya kaboni na kuboresha mifumo ya Upimaji, Utoaji wa Taarifa na Uhakiki (MRV) ili kuongeza uwazi na kuimarisha imani ya wawekezaji.

Aidha, alisema Kituo hicho kinapaswa kuhakikisha manufaa yatokanayo na miradi ya kaboni yanagawanywa kwa haki, hasa kwa jamii zinazoshiriki katika uhifadhi wa mazingira, huku kikijenga uwezo wa wataalamu wa ndani katika mnyororo mzima wa thamani wa biashara ya kaboni.

“Tanzania lazima ijenge mfumo wa soko la kaboni unaovutia uwekezaji, unaolinda uadilifu wa mazingira na kuhakikisha wananchi wananufaika na fursa zinazotokana na sekta hii,” alisema.

Alisema usimamizi madhubuti wa sekta ya kaboni utachangia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kwa kuongeza mapato ya Serikali, kuvutia uwekezaji wa kijani, kuimarisha ustahimilivu wa jamii dhidi ya mabadiliko ya tabianchi na kuchochea maendeleo endelevu.

Katika hatua nyingine, Dkt. Muyungi aliitaka Menejimenti ya Kituo Cha Kaboni kukamilisha kwa haraka mifumo muhimu ya uendeshaji, ikiwemo kuboresha Mfumo wa Usajili wa Kaboni (Carbon Registry), kuwasilisha Mpango Mkakati wa Kituo na kuimarisha mifumo ya kitaasisi.

Pia aliitaka bodi ya Kituo hicho kuandaa taarifa ya kina kuhusu miradi yote ya kaboni iliyosajiliwa na ile iliyoanza utekelezaji kati ya Januari na Julai 2026, ikionesha hatua iliyofikiwa, kiwango cha uwekezaji na manufaa yanayotarajiwa kwa Taifa na wananchi.

Mwenyekiti wa Bodi ya Kituo cha Kaboni, Dkt. Albina Chuwa, ameahidi kutekeleza maelekezo hayo na kuongeza uelewa wa umma kuhusu biashara ya kaboni nchini, sambamba na kuimarisha utawala bora katika sekta hiyo.

Kituo cha Kaboni kilianzishwa kupitia marekebisho ya Sheria ya Usimamizi wa Mazingira kwa lengo la kuratibu ufuatiliaji wa kaboni, kuimarisha usimamizi wa masoko ya kaboni na kuiwezesha Tanzania kushiriki kikamilifu katika fursa za fedha za tabianchi duniani.








Na Janeth Raphael - MichuziTv 

Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dodoma, imeamuru Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), Melkisedeki Kaijage, aachiwe kwa dhamana kuanzia Julai 21, 2026, wakati uchunguzi wa tuhuma za uchochezi zinazomkabili ukiendelea.

Uamuzi huo umetolewa na Jaji Joachim Tiganga wakati wa usikilizwaji wa Shauri Na. 15653/2026.

Kaijage amekuwa akishikiliwa katika Kituo cha Polisi Chang’ombe akituhumiwa kuhamasisha maandamano yaliyojulikana kama “Sabasaba.”

Wakati wa usikilizwaji wa maombi hayo, upande wa Serikali uliieleza Mahakama kuwa haukuwa na pingamizi dhidi ya ombi la dhamana, na kwamba taratibu za kumwachia mshtakiwa zinaweza kuendelea kwa mujibu wa sheria.

Wakili wa Kaijage, Prosper Malangalila, alidai kuwa mteja wake alikaa mahabusu kwa siku 12 bila kufikishwa mahakamani, licha ya kosa analotuhumiwa kuwa la dhamana. Aliiomba Mahakama iamuru mteja wake aachiwe kwa dhamana, alipwe fidia kwa kuzuiliwa kwa muda huo, na Serikali ilipe gharama za maombi hayo.

Baada ya kusikiliza hoja za pande zote, Mahakama ilikubali ombi la dhamana na kuamuru Kaijage aachiwe kwa masharti ya dhamana. Hata hivyo, ilikataa ombi la kulipwa fidia kwa kipindi alichokuwa mahabusu.

Mahakama imeeleza kuwa baada ya uchunguzi kukamilika, Kaijage atafikishwa mahakamani kujibu rasmi tuhuma zinazomkabili.

Akizungumza nje ya Mahakama, Wakili Prosper Malangalila amesema upande wake umepokea uamuzi huo na utaendelea kufuatilia hatua zinazofuata za kisheria katika shauri hilo.





Njedengwa - Dodoma 📍

SERIKALI inaendelea na utekelezaji wa mkakati wake wa kuongeza tija katika kilimo baada ya kusambaza pampu za Umwagiliaji kwa vikundi vya wakulima na kuchimba visima 390 katika mikoa 15, hatua inayotarajiwa kuwawezesha wakulima kulima mwaka mzima na kuongeza uzalishaji wa mazao.

Hatua hiyo itawanufaisha wakulima 15,022 kupitia vikundi 769, huku eneo la ekari 13,518.75 likitarajiwa kuingia kwenye kilimo cha umwagiliaji na kupunguza utegemezi wa mvua.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma, Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji (NIRC), Raymond Mndolwa, alisema pamoja na Tume kuendelea na ujenzi wa miradi ya Umwagiliaji na ile ya kimkakati pia inaendelea kutekeleza kwa vitendo mkakati wake wa kuongeza tija katika kilimo kwa kusambaza pampu za Umwagiliaji kwa vikundi vya wakulima na kuchimba visima 390 katika mikoa 15.

Hatua hiyo inatarajiwa kuwawezesha wakulima kulima mwaka mzima na kuongeza uzalishaji wa mazao.

Alisema, mpango huo unatekeleza maelekezo ya Serikali ya kuwawezesha wakulima wenye mashamba madogo kujikwamua kiuchumi hususani wanawake na vijana kwa kupata uhakika wa maji.

"Tumeelekezwa kutafuta njia zitakazowawezesha wananchi wa kipato cha chini kujiongezea kipato. Ndiyo maana pamoja na miradi mikubwa ya Umwagiliaji, tumeanza uchimbaji wa visima na ugawaji wa pampu kwa wakulima wadogo," alisema.

Alisema pampu hizo ni maalumu kwa wakulima wanaolima karibu na mito na maziwa ili kuwasaidia kufanya kilimo kinachohifadhi mazingira na kuongeza uzalishaji.

Mndolwa alisema kati ya pampu 2,000 zilizonunuliwa na Serikali, pampu 1,000 tayari zimepokelewa na kupelekwa katika mikoa ya Mwanza, Mara, Kagera, Kigoma, Simiyu, Geita na Katavi kwa ajili ya kuanza kutumika.

Alisema pampu hizo zitagawiwa kwa vikundi 769 vya wakulima na kunufaisha wanawake 6,335 na wanaume 8,702, hivyo kufikisha jumla ya wanufaika 15,022.

"Pampu hizi zitawasaidia wakulima kuondokana na utegemezi wa mvua na kuwawezesha kulima misimu yote ya mwaka, jambo litakaloongeza uzalishaji na kipato chao," alisema.

Mndolwa alisema hadi sasa Tume imechimba visima 390 katika mikoa 15, ambapo Dodoma inaongoza kwa visima 93, ikifuatiwa na Manyara na Tabora zenye visima 44 kila mmoja, Geita 42, Singida 32, Njombe 30, Tanga 22, Iringa 20, Mara na Morogoro visima 17 kila mmoja.

Alitaja mikoa mingine iliyonufaika ni Pwani na Arusha zenye visima 10 kila mmoja, Mtwara nane, Mbeya saba na Ruvuma visima vitano.

Alisema Serikali pia imeanza ununuzi wa pampu 500 kwa ajili ya visima hivyo, ambapo pampu 100 tayari zimepokelewa, nyingine 100 ziko njiani kutoka kwa mtengenezaji na pampu 300 zipo katika hatua za manunuzi.

Mbali na pampu hizo, alisema Serikali inatarajia kupokea pampu nyingine 1,000 zinazotumia nishati ya jua ambazo zitasambazwa katika maeneo yenye changamoto ya upatikanaji wa umeme ili kuongeza wigo wa kilimo cha umwagiliaji.

Alifafanua kuwa visima vinachimbwa kwenye mashamba ya wakulima baada ya kuunganishwa katika vikundi, lakini hubaki kuwa mali ya umma ili wanakikundi wote wanufaike kwa usawa na kuhakikisha huduma hiyo inadumu.

Aidha, alisema vikundi vyote vinavyonufaika husajiliwa kwa mujibu wa sheria ili kurahisisha usimamizi wa miradi hiyo pamoja na ukusanyaji wa mapato ya Serikali.

Mndolwa alisema utekelezaji wa mradi huo unatarajiwa pia kutoa ajira kwa zaidi ya vijana 4,000 watakaoshiriki katika ufungaji, uendeshaji na usimamizi wa mifumo ya Umwagiliaji, huku akisisitiza kuwa lengo la Serikali ni kuhakikisha Umwagiliaji unakuwa chachu ya mapinduzi ya kilimo, usalama wa chakula na ukuaji wa uchumi wa wananchi.




Top News