Wakati dunia ikiadhimisha Siku ya Kimataifa ya Bia leo, Serengeti Breweries Limited (SBL) inaungana na maadhimisho hayo kwa namna ya kipekee baada ya bidhaa zake kuthibitika kuwa na viwango vya kimataifa. Mafanikio hayo yamekuja kufuatia Serengeti Lite, Serengeti Lager na Serengeti Lemon kutunukiwa Tuzo za Gold Quality Awards 2026 kutoka taasisi maarufu duniani ya Monde Selection.
Tuzo za Gold Quality Awards zinazotolewa na Monde Selection hutolewa kwa bidhaa zinazokidhi viwango vya juu vya ubora vinavyotambulika kimataifa baada ya kupitia mchakato makini wa tathmini unaofanywa na jopo huru la wataalamu wa kimataifa. Bidhaa hupimwa kwa kuzingatia vigezo mbalimbali ikiwemo ubora wa jumla, ladha, mwonekano, ubunifu, taarifa kwa watumiaji pamoja na uzoefu wa mtumiaji, ili kuhakikisha zinakidhi viwango vinavyotambulika duniani.
Monde Selection ilianzishwa mwaka 1961 mjini Brussels, Ubeligiji, ikiwa ni taasisi huru ya kimataifa inayojihusisha na tathmini ya ubora wa bidhaa za walaji. Kwa zaidi ya miaka 65, taasisi hiyo imekuwa ikitathmini maelfu ya bidhaa katika makundi mbalimbali, ikiwemo vyakula, bia, vinywaji vikali, bidhaa za afya na lishe pamoja na vipodozi. Kila mwaka, tathmini hizo hufanywa na wataalamu zaidi ya 80 kutoka mataifa mbalimbali, huku bidhaa kutoka takribani nchi 150 zikiwa zimewasilishwa kwa ajili ya kufanyiwa tathmini kwa kipindi chote.
Mafanikio haya yanaakisi dhamira endelevu ya Kampuni ya Serengeti ya kuzalisha vinywaji vya ubora wa kiwango cha kimataifa kupitia uwekezaji unaoendelea katika teknolojia za kisasa za uzalishaji, mifumo madhubuti ya uhakiki wa ubora, pamoja na ubunifu unaomweka mlaji katika kitovu cha kila hatua ya shughuli zake.
Akizungumzia mafanikio hayo, Mkurugenzi wa Ugavi wa SBL Joseph Cheloti, alisema tuzo hizo ni uthibitisho wa dhamira kuu ya kampuni katika kuhakikisha bidhaa zake zinadumisha viwango vya juu vya ubora.
"Kupokea Tuzo za Gold Quality Awards kutoka Monde Selection ni heshima kubwa na uthibitisho kuwa bidhaa zetu zinakidhi viwango vya ubora vinavyotambulika kimataifa. Tunajivunia mafanikio haya ambayo yanadhihirisha kujitolea kwa wafanyakazi wetu, ubora wa malighafi tunazotumia pamoja na uimara wa mifumo yetu ya uzalishaji. Zaidi ya yote, tunawashukuru wateja wetu kwa kuendelea kutuamini na kutuunga mkono."
Aliongeza kuwa kampuni itaendelea kuwekeza katika ubora, ubunifu na maendeleo ya bidhaa ili kuhakikisha watumiaji nchini Tanzania na katika masoko mengine wanaendelea kupata vinywaji vinavyokidhi viwango vya juu vya ubora duniani.
Mbali na bidhaa hizo tatu za bia, chapa ya vinywaji vikali ya kampuni hiyo, TZEE, pia ilitunukiwa Tuzo ya Gold Quality Award 2026. Kupokea Tuzo nne za Gold Quality Awards kwa wakati mmoja kunazidi kuimarisha nafasi ya Kampuni hiyo, kama miongoni mwa wazalishaji wa vinywaji wanaozingatia ubora unaotambulika kimataifa, huku ikiendelea kuipeperusha bendera ya Tanzania na kuonesha ubora wa bidhaa zake katika jukwaa la dunia.
Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) wa CCM, Idara ya Organizesheni, Paul Chacha amesema uongozi wake utasimamia uchaguzi wa haki na usawa ndani ya chama, akisisitiza kuwa hakuna mwanachama atakayepokonywa haki yake kutokana na ushawishi wa fedha au mamlaka ya watu binafsi.
Akizungumza katika makao makuu ya CCM jijini Dodoma wakati wa mapokezi ya viongozi wapya walioteuliwa kushika nyadhifa mbalimbali ndani ya chama, Chacha amesema CCM ndiyo chama kilichojipanga zaidi nchini na kinaendelea kuwahakikishia Watanzania amani, maendeleo na matumaini ya maisha bora.
Amesema uchaguzi ndani ya chama unapaswa kuwa wa haki na uwazi ili kumpata kiongozi anayestahili kwa ridhaa ya wanachama, huku akiahidi kusimama imara kulinda misingi ya demokrasia bila kuyumbishwa na shinikizo lolote.
Chacha ametoa onyo kwa watu wanaokusudia kutumia fedha kujinufaisha kisiasa, akisema ni heri fedha hizo zikaelekezwa kwenye uwekezaji au biashara kuliko kutumika kuwarubuni wapiga kura.
Aidha, amesisitiza kuwa CCM haitamvumilia mtu yeyote atakayejaribu kununua kura au kushawishi wanachama kwa fedha ili kupata nafasi za uongozi, akibainisha kuwa hatua kali zitachukuliwa kwa wote watakaokiuka maadili ya chama.
Vilevile, amesema chama hakitasita kuwachukulia hatua watu wanaotumia nafasi au mamlaka ya ndugu zao kuingilia mchakato wa uchaguzi na kutoa maelekezo yanayokandamiza haki za wanachama.
Kwa mujibu wa Chacha, uchaguzi wa haki ndio msingi wa kupata viongozi wenye uwezo wa kukijenga chama na kuendelea kuwatumikia Watanzania kwa uadilifu na uwajibikaji.
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Hamad Chande, ameipongeza Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) kwa mchango wake katika kuwawezesha wakulima kupata masoko yenye ushindani kupitia Mfumo wa Stakabadhi za Ghala.
Mhe. Chande ameyasema hayo leo Agosti 6, 2026, baada ya kutembelea banda la WRRB katika Maonesho ya 88 yanayoendelea katika Viwanja vya Dkt. John Malecela, jijini Dodoma.
Amesema WRRB imeendelea kuwa nyenzo muhimu katika kuimarisha biashara ya mazao kwa kuwawezesha wakulima kupata masoko yenye ushindani, kuongeza thamani ya mazao yao na kuchangia ukuaji wa uchumi wa taifa.
Aidha, ameipongeza WRRB kwa kuendelea kutoa elimu kwa wananchi na kutoa wito kwa wadau wa sekta ya kilimo kuendelea kutekeleza kwa vitendo kauli mbiu ya Maonesho ya Nane Nane ya mwaka 2026 isemayo, "Tambua Soko, Ongeza Tija, Tekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050," kwa kuimarisha mifumo ya masoko, kuongeza tija katika uzalishaji na kuhakikisha wakulima wananufaika na fursa zilizopo katika mnyororo wa thamani wa mazao.
Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Uratibu Huduma ,Bw. Mwita Thomas ameeleza kuwa WRRB itaendelea kuboresha huduma zake, kuimarisha usimamizi wa mfumo huo kwa kushirikiana na wadau ili kuhakikisha sekta ya kilimo inakuwa chachu ya maendeleo ya uchumi na ustawi wa wananchi.

DODOMA Mfumo wa kuagiza mafuta kwa ajili ya matumizi ya miezi miwili inayofuata umeiwezesha Tanzania kuendelea kuwa na bidhaa za mafuta za kutosha, licha ya vita na changamoto nyingine zinazoathiri soko la dunia.
Hayo yameelezwa na Mhandisi Rehema Mahundi katika siku ya sita ya Maonesho ya Nanenane yanayoendelea jijini Dodoma, wakati akitoa elimu kwa wananchi waliotembelea Banda la Wakala wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (PBPA).
Mhandisi Mahundi alisema moja ya maswali yanayoulizwa zaidi na wananchi ni namna Mfumo wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja unavyoiwezesha nchi kuwa na uhakika wa upatikanaji wa mafuta, hasa wakati wa migogoro na vita katika maeneo mbalimbali duniani.
Akijibu swali hilo, alieleza kuwa PBPA hutangaza zabuni kila mwezi kwa ajili ya kuagiza mafuta yatakayotumika nchini katika miezi miwili inayofuata. Utaratibu huo unajulikana kama M+2.
“PBPA huingia mikataba na wazabuni walioshinda zabuni hizo ili kuhakikisha bidhaa za mafuta zinafika nchini kwa wakati, hata changamoto zinapojitokeza katika soko la dunia,” alisema Mhandisi Mahundi.
Alisema kupitia mfumo huo, Tanzania imeendelea kuwa na uhakika wa upatikanaji wa mafuta wakati wote na kwa gharama zinazoakisi hali halisi ya soko la dunia.
Katika Maonesho ya Nanenane, PBPA imeendelea kutoa elimu kuhusu Mfumo wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja kwa watu kutoka makundi mbalimbali, wakiwamo wanafunzi, wakulima, wajasiriamali, wafanyabiashara pamoja na wawakilishi kutoka taasisi za elimu na sekta binafsi.
Mhandisi Mahundi amewakaribisha wananchi kutembelea Banda la PBPA katika Viwanja vya Nanenane jijini Dodoma ili kupata elimu zaidi kuhusu namna mfumo huo unavyosimamia mnyororo wa uagizaji, usimamizi na upokeaji wa bidhaa za mafuta nchini.


Na Mwandishi Wetu
RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk.Samia Suluhu Hassan na Yoweri Museveni wa Uganda wameshuhudia utiaji saini wa Hati ya Makubaliano (MoU) ya kuendeleza ujenzi wa kiwanda cha kusafisha mafuta na Kitovu cha Nishati cha Kikanda Jijini Tanga, mradi unaotarajiwa kubadili taswira ya sekta ya nishati Afrika Mashariki.
Makubaliano hayo yaliyosainiwa na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), Kampuni ya Taifa ya Mafuta ya Uganda (UNOC) na kampuni ya VTTO Bahrain, yanafungua njia kwa hatua za awali za kitaalamu na uwekezaji katika ujenzi wa miundombinu hiyo muhimu.
Akizungumza katika hafla hiyo,leo Ikulu jijini Dar es Salaam Waziri wa Nishati Deogratias Ndejembi alisema makubaliano hayo ni hatua muhimu katika kuimarisha ushirikiano wa Tanzania na Uganda kwenye sekta ya nishati.
Njejembi amesema kuwa mradi huo unatarajiwa kujumuisha kiwanda cha kusafisha mafuta, miundombinu ya kuhifadhi bidhaa za petroli, huduma za usafirishaji pamoja na bomba la kusafirisha bidhaa za mafuta linaloweza kufanya kazi kwa pande zote mbili kati ya Tanzania na Uganda.
Amesema kuwa utekelezaji wa mradi huo unalenga kuifanya Tanga kuwa kituo muhimu cha usambazaji wa bidhaa za mafuta kwa nchi za Afrika Mashariki na ukanda mpana wa Afrika.
"Utiaji saini wa leo siyo tu makubaliano, bali ni msingi mwingine wa mageuzi ya kiuchumi katika Afrika Mashariki," alisema.
Alisema mradi huo unaendeleza ushirikiano ulioanza kupitia Mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP), wenye thamani ya takribani dola za Marekani bilioni sita, unaolenga kusafirisha mafuta ghafi kutoka maeneo ya uzalishaji nchini Uganda hadi Bandari ya Tanga.
Ndejembi alisema tofauti na EACOP ambayo inalenga kusafirisha mafuta ghafi, Kitovu cha Nishati cha Tanga kitasaidia kuongeza thamani ya rasilimali hiyo kupitia usafishaji wa mafuta, uhifadhi, usafirishaji na biashara ya bidhaa za petroli.
"Mradi huu ukikamilika una uwezo wa kuvutia uwekezaji unaozidi dola za Marekani bilioni 20, kuunda ajira, kuchochea ukuaji wa viwanda na kuimarisha usalama wa nishati katika ukanda huu," alisema.
Ndejembi aliongeza mradi huo unaendana na maono ya Rais Samia ya kuifanya Tanga kuwa kitovu cha biashara ya mafuta Afrika Mashariki kutokana na nafasi yake ya kimkakati, ikiwemo kuwa lango la Bahari ya Hindi na eneo la kupokea bomba la EACOP.
Kwa upande wake, Waziri wa Nishati na Maendeleo ya Madini wa Uganda, Dk Ruth Nankabirwa Ssentamu, alisema makubaliano hayo yanaonyesha dhamira ya nchi hizo mbili ya kushirikiana katika kuongeza thamani ya rasilimali na kukuza uchumi wa kikanda.
"Hatupaswi kuuza malighafi pekee. Tunapaswa kujenga viwanda, kuunda ajira zenye ujuzi na kuhakikisha wananchi wetu wanapata manufaa makubwa kutokana na rasilimali hizi," alisema.
Dk Nankabirwa alisema kiwanda cha kusafisha mafuta kinachopangwa kujengwa Kabaale nchini Uganda na Kitovu cha Nishati cha Tanga havitashindana, bali vitakamilishana kwa kuongeza uwezo wa usafishaji wa mafuta na kuimarisha upatikanaji wa nishati katika Afrika Mashariki.
Aliongeza kuwa Tanzania na Uganda zinaendelea na utekelezaji wa miradi mingine ya pamoja, ikiwemo bomba la kusafirisha bidhaa za mafuta, bomba la gesi asilia kati ya nchi hizo mbili na mradi wa njia ya kusafirisha umeme wa kilovolti 400.
Utiaji saini wa makubaliano hayo ni hatua nyingine katika ushirikiano wa muda mrefu wa Tanzania na Uganda kwenye sekta ya nishati ulioimarishwa kupitia EACOP mwaka 2017.



.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)


.jpeg)

.jpeg)


.jpeg)



.jpeg)





.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)
