Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Ukaguzi na Usimamizi wa Vyama vya Ushirika Tanzania (COASCO), CPA Jeremia Jackson Mugeta, amesema shirika hilo limepokea na liko tayari kutekeleza maagizo yaliyotolewa na Makamu wa Rais, Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, ya kuhakikisha linavikagua na kuvisimamia vyama vya ushirika pamoja na kuwasilisha taarifa kuhusu hali ya ushirika nchini.
CPA Mugeta amesema hayo alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya maadhimisho ya Siku ya Ushirika yaliyofanyika katika Kijiji cha Ushirika ndani ya viwanja vya Maonesho ya Nanenane kitaifa jijini Dodoma Agosti 3, 2026.
Ameeleza kuwa katika mwaka wa fedha 2026/2027 shirika hilo lilianza maandalizi ya ukaguzi kuanzia Julai 20 kwa kuandaa mpango kazi, huku wataalamu wakiendelea kuratibu zoezi hilo ambalo litahusisha vyama vyote vya ushirika vilivyofunga hesabu zake Machi 31, 2026.
Amefafanua kuwa kwa mujibu wa sheria, vyama vya ushirika vinapofunga hesabu zake hupewa miezi mitatu kuandaa na kuwasilisha taarifa za fedha kwa mkaguzi wa nje ambaye ni COASCO, na kwamba mara baada ya maonesho ya Nanenane wakaguzi wataanza kwenda katika maeneo ya vyama hivyo kwa ajili ya kufanya ukaguzi.
CPA Mugeta amesema COASCO itatekeleza maagizo yote yaliyotolewa na Makamu wa Rais na kuwasilisha taarifa kwa mamlaka husika kulingana na ratiba ya kisheria, ambapo ripoti ya kwanza itawasilishwa mwezi Januari 2027 kwa Waziri wa Kilimo baada ya kukamilika kwa kipindi cha miezi sita.
Amesema katika mwaka wa fedha uliopita COASCO ilikuwa na lengo la kukagua takribani vyama 5,000 vya ushirika, ambapo ilifanikiwa kukagua vyama 4,858, huku lengo la mwaka wa fedha 2026/2027 likiwa ni kukagua vyama vyote vya ushirika nchini.
Aidha, ametoa wito kwa vyama vya ushirika kuzingatia sheria kwa kufunga hesabu zao kwa wakati na kuziwasilisha kwa COASCO kwa ajili ya ukaguzi.
Amesisitiza kuwa mafanikio ya zoezi hilo yanategemea ushirikiano wa kila chama cha ushirika kutekeleza wajibu wake kwa mujibu wa sheria, akionya kuwa vyama vitakavyokiuka taratibu na sheria vitachukuliwa hatua na Mrajis wa Vyama vya Ushirika.






.jpeg)

.jpeg)



.jpeg)
.jpeg)


.jpeg)



.jpeg)






.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)



