▪️Awataka watumishi kutimiza wajibu wao

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amewahimiza watendaji wa Serikali kuwahudumia kikamilifu Watanzania ili miradi inayojengwa na Serikali itoe matokeo chanya.

“Tunachokijenga hapa, si jengo pekee, bali tunajenga mazingira bora ya utendaji wa mfuko. Kupitia uwekezaji huu tunachochea na tunaharakisha utekelezaji wa dhamira ya dhati aliyoionesha Mheshimiwa Rais kumsaidia mkulima mdogo kwa kuwezesha kupata mikopo.”

“Watumishi wote wanapaswa kutimiza wajibu wao kwa bidii ili uwekezaji huu uwe na manufaa kwa Taifa. Tusiweke ofisi nzuri halafu huduma zikawa duni, tutakua hatujafikia malengo yaliyokusudiwa, ofisi nzuri lakini mwananchi akija kupata huduma anaambiwa njoo kesho, njoo kesho, majengo haya hayatakuwa na maana,” amesema Waziri Mkuu.

Waziri Mkuu ameyasema hayo leo (Jumapili Agosti 2, 2026) Iyumbu jijini Dodoma wakati akiweka jiwe la msingi la ujenzi wa makao makuu ya ofisi za Mfuko wa Udhamini wa Pembejeo za Kilimo (AGITF).

Dkt. Mwigulu amesisitiza kuwa uwekezaji huo unaofanywa na Serikali katika utafiti wa kilimo ni mwelekeo sahihi wa mageuzi katika sekta ya kilimo. “Kuwekeza kwenye utafiti ni njia sahihi ya kufanya mageuzi katika sekta husika, tumetoka kufanya uzinduzi wa makao makuu ya taasisi yetu ya utafiti wa kilimo, na pembeni yake kuna jengo zuri la maabara ya kilimo, kuonesha jinsi Rais anamaanisha kwa dhati kufanya mageuzi katika kilimo.”

“Kwa nchi nyingine maabara ile ya kisasa ingekuwa kwenye moja ya chuo kikuu, lakini ile ni maabara ya wizara na ipo hapa makao makuu ya nchi,” ameongeza Waziri Mkuu.

Awali akiwa katika mji wa Serikali - Mtumba, kwenye halfa ya uwekaji wa jiwe la msingi la ujenzi wa ofisi za makao makuu ya Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI), Waziri Mkuu alimpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendeleza uwekezaji jijini Dodoma hali iliyochochea ukuaji wa mkoa huo.

Dkt. Mwigulu ameongeza kuwa hatua hiyo ya Rais Samia imeenda sambamba na kuwaamini wakandarasi wazawa jambo lililowakuza wakandarasi hao.

“Mheshimiwa Rais aliweka imani kwao, akasema waacheni wajenge. Tumeona majengo na miradi ikimeremeta….nilipita katika miradi ya sekta nyingine, nikakuta madaraja yenye urefu wa ghorofa yamejengwa na wakandarasi wazawa, zaidi ya madaraja 81, sasa ukiangalia kwa jicho la kibinafsi utasema si ni yule mmoja tu ndiyo akapata mradi, lakini niwaambieni huo ni mzunguko wa uchumi wa ndani ya nchi, ndiyo maana mabenki yanapata wateja na yamepunguza mikopo chechefu,” amesisitiza Waziri Mkuu.

Mapema, akimkaribisha Waziri Mkuu, Waziri wa Kilimo, Daniel Chongolo amemshukuru Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuiwezesha wizara hiyo kupata bajeti ya kutosha kuendesha shughuli zake, ikiwemo kuwaongezea bajeti kila mwaka.














NA DENIS MLOWE - DAR ES SALAAM

VICTORIA Group (VG) imetangaza kuandaa mbio za afya za VG Fun Run zitakazofanyika Agosti 8, 2026 katika viwanja vya Victoria Park, Ununio jijini Dar es Salaam, zikiwa na lengo la kuhamasisha afya, kuimarisha mshikamano wa wanachama na kuwashirikisha wananchi katika mazoezi ya mwili.

Akizungumza na waandishi wa habari, Mwenyekiti wa Kamati ya VG Fun Run, Isidori Msaki, alisema wazo la kuanzisha mbio hizo limetokana na ukweli kuwa Victoria Group imekuwa pamoja kwa zaidi ya miaka 26 na sasa wanachama wengi wamefikisha umri wa zaidi ya miaka 50, jambo lililowasukuma kuweka kipaumbele kwenye afya zao.

Alisema Victoria Group ina wanachama 113 ambao pamoja na familia zao wanafikia takribani watu 700, hivyo wameona ni muhimu kuanzisha shughuli ya pamoja itakayowahamasisha kufanya mazoezi na kuishi maisha yenye afya.

Msaki alisema mbio hizo zitahusisha kukimbia umbali wa kilomita 10 kuanzia saa 12:00 asubuhi, huku washiriki wote watakaomaliza wakitunukiwa medali na kuandaliwa huduma ya supu, wakati wadhamini wa tukio watapatiwa vyeti vya shukrani kwa mchango wao.

Alisema tukio hilo halitawahusu wanachama wa Victoria Group pekee, bali pia limefunguliwa kwa marafiki na wananchi wote wanaotaka kushiriki.

Msaki alisema washiriki kutoka nje ya Victoria Group watatakiwa kulipa shilingi 30,000 ambazo zitajumuisha fulana maalumu, namba ya ushiriki pamoja na medali baada ya kumaliza mbio.

Aliongeza kuwa kwa wale wasioweza kushiriki mbio za kilomita 10, waandaaji wameandaa programu maalumu ya mazoezi ya aerobics itakayofanyika katika Victoria Park chini ya wakufunzi wa mazoezi, sambamba na burudani ya muziki na shughuli nyingine za kijamii.

Msaki alisema hadi sasa zaidi ya washiriki 126 wamekwishajisajili, huku matarajio yakiwa kufikisha zaidi ya washiriki 200 kabla ya siku ya tukio.

Naye Mwenyekiti wa Victoria Group, Sabasaba Mushingi, alisema kikundi hicho kilianzishwa takribani miaka 26 iliyopita kwa lengo la kujenga mshikamano na kusaidiana katika nyakati za furaha na huzuni, lakini kadiri miaka ilivyokwenda wamepanua shughuli zao hadi kwenye uwekezaji wa kiuchumi.

Alisema kwa sasa Victoria Group inamiliki vitega uchumi mbalimbali ikiwemo Victoria Park yenye thamani inayokadiriwa kuzidi shilingi bilioni moja kwa tathmini ya sasa, pamoja na uwekezaji katika hati fungani za Serikali na hisa.
Mushingi alisema VG Fund Run ni mwanzo wa safari ya kulifanya tukio hilo kuwa moja ya mbio kubwa nchini, zitakazokuwa zikifanyika kila mwaka na kuvutia washiriki wengi zaidi kutoka ndani na nje ya Victoria Group.

Alieleza kuwa baada ya tathmini ya tukio la mwaka huu, uongozi unapanga kuliboresha zaidi ili katika miaka ijayo liwe na zawadi kubwa, washiriki wengi zaidi na pia liwe jukwaa la kuchangisha fedha kwa ajili ya kusaidia jamii kupitia miradi mbalimbali ya kijamii.

Aliwahimiza wananchi kujitokeza kwa wingi Agosti 8 katika Victoria Park, Ununio, kushiriki siku ya mazoezi, afya na burudani, akisisitiza kuwa lengo kuu la Victoria Group ni kujenga jamii yenye afya bora huku ikiendeleza mshikamano na utamaduni wa kusaidiana.






Chama Kikuu cha Ushirika Tunduru (TAMCU) kimetangaza kufunguliwa kwa msimu mpya wa ununuzi wa zao la mbaazi utakaoanza katikati ya mwezi Agosti, huku kikieleza kuwa kimejipanga kuhakikisha uzalishaji unaongezeka na wakulima wanalipwa kwa wakati kupitia mfumo wa stakabadhi za ghala.

Akizungumza na waandishi wa habari Agosti 2, 2026, katika Maonesho ya Kilimo Nanenane Kitaifa, Mjumbe wa Bodi ya TAMCU, Nurdin Raisi Chakilo, alisema chama hicho tayari kimefunga msimu wa zao la ufuta na sasa kinaelekeza nguvu katika maandalizi ya msimu wa mbaazi.

Alisema TAMCU imejipanga kuhakikisha mnyororo mzima wa mfumo wa stakabadhi za ghala unafanya kazi kwa ufanisi, huku ikiwahamasisha wakulima kukusanya mazao yao, kuyaandaa kwa ubora na kuyapeleka kwenye maghala ya mnada ili kupata soko na malipo kwa wakati.

Chakilo alisema chama hicho kinajivunia mafanikio ya mfumo huo kutokana na minada kufanyika kwa wakati na wakulima kulipwa kwa wakati, hali iliyoongeza uelewa na imani ya wakulima katika mfumo wa stakabadhi za ghala.

Aidha, alisema TAMCU imeongeza thamani ya mali zake kutoka shilingi bilioni 1.5 hadi kufikia shilingi bilioni 5, sambamba na kuanzisha mradi wa usafirishaji wa mazao na mizigo mchanganyiko unaotoa huduma katika maeneo mbalimbali nchini kwa kutumia magari yenye uwezo wa kubeba tani 32 kwa kila safari.

Aliongeza kuwa chama hicho kimejipanga kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kupitia mpango wa kujenga kiwanda cha korosho wilayani Tunduru pamoja na jengo la utawala lenye ghorofa tano litakalokuwa na ukumbi wa watu zaidi ya 700, ofisi za TAMCU na maeneo ya kupangisha.

Chakilo alisema TAMCU, inayohudumia vyama vya msingi Wilayani Tunduru Mkoani Ruvuma pamoja na baadhi ya wakulima wa mkoa jirani wa Njombe kwa zao la korosho, kimeendelea kunufaika na jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita kupitia upatikanaji wa pembejeo za kilimo, hatua iliyochangia kuongeza tija katika uzalishaji wa mazao.


Kampuni ya mawasiliano ya Yas Tanzania imezindua rasmi mnara wa 5G wilayani Masasi, Mkoa wa Mtwara, hatua inayotarajiwa kuongeza kasi ya biashara, kuboresha upatikanaji wa huduma za kidijitali na kufungua fursa mpya za maendeleo kwa wakazi wa wilaya hiyo na maeneo ya jirani.

Uwekezaji huo ni sehemu ya mkakati wa Yas wa kuendelea kusogeza teknolojia ya kisasa karibu na wananchi ili kuwawezesha kunufaika na uchumi wa kidijitali kupitia mawasiliano yenye kasi, uhakika na ubora.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mkuu wa Yas Kanda ya Pwani Kusini, Bi. Fadhila Saidi, alisema kampuni inaendelea kuwekeza katika miundombinu ya kisasa ya mawasiliano ili kuhakikisha Watanzania wanapata suluhisho zinazowawezesha kuboresha maisha na kukuza shughuli zao za kiuchumi.

"Tunazindua mnara huu wa 5G kwa lengo la kuhakikisha wakazi wa Masasi na mkoa wa Mtwara kwa ujumla wanapata huduma za mawasiliano zenye kasi na ubora ili kuchochea shughuli za kiuchumi na mawasiliano ya uhakika. Kwetu sisi, teknolojia ni nyenzo ya kuwawezesha Watanzania kufikia fursa zaidi za maendeleo," alisema Bi. Saidi.

Aliongeza kuwa, Wilaya ya Masasi ina wakazi zaidi ya 315,000 wanategemea kilimo na biashara, hivyo uzinduzi wa teknolojia ya 5G wilayani humo utachochea shughuli mbalimbali za kimaendeleo, kwani wakulima wataweza kufuatilia bei za mazao na kuwasiliana moja kwa moja na masoko, huku wafanyabiashara wakipanua biashara zao kupitia majukwaa ya kidijitali na mifumo ya kisasa ya malipo”.

Bi. Saidi alisema huduma hiyo pia itawanufaisha vijana kwa kuwafungulia fursa za ajira, ubunifu na ujasiriamali kidijitali, huku wanafunzi na walimu wakipata urahisi wa kutumia majukwaa ya kujifunzia mtandaoni. Aidha, taasisi za afya na huduma nyingine za kijamii zitanufaika na mawasiliano yenye kasi na uhakika yatakayoongeza ufanisi katika utoaji wa huduma.

Aliongeza kuwa, sambamba na uwekezaji katika mawasiliano, kwa upande wa Mixx, Kampuni inaendelea kuwawezesha wananchi kutuma na kupokea fedha, kulipa bili, kufanya malipo ya biashara na kupata huduma mbalimbali za kifedha kwa usalama na urahisi, hatua inayochochea ujumuishaji wa kifedha na ukuaji wa uchumi wa wananchi.

Kwa upande wake, mkazi wa Masasi na mfanyabiashara, Bw. Jaffari Wadi, alisema uzinduzi wa mnara huo wa 5G utakuwa chachu ya kukuza biashara katika eneo hilo.

"Uzinduzi wa mnara huu wa 5G utatusaidia kwa kiasi kikubwa kuchochea ukuaji wa biashara zetu kwani huduma sasa zitakuwa za haraka zaidi. Tutakuwa na uwezo wa kuwasiliana kwa urahisi na wateja, kufanya miamala kwa wakati na kutumia fursa za biashara mtandaoni ambazo hapo awali zilikuwa changamoto kutokana na kasi ya mtandao," alisema Bw. Wadi.

Yas imeendelea kuwekeza katika upanuzi wa mtandao wake nchini ikiwa ni sehemu ya dhamira yake ya kuhakikisha hakuna Mtanzania anayebaki nyuma katika safari ya mageuzi ya kidijitali. Kampuni hiyo inaamini kuwa upatikanaji wa miundombinu ya mawasiliano yenye ubora ni msingi wa kukuza biashara, kuimarisha ujumuishaji wa kidijitali na kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Uzinduzi wa mnara wa 5G Masasi unaongeza hatua nyingine katika juhudi za Yas za kuendelea kuwapatia Watanzania suluhisho za mawasiliano na kifedha zinazowawezesha kufungua fursa mpya za maendeleo na kushiriki kikamilifu katika uchumi wa kidijitali.
Mkuu wa Yas Kanda ya Kusini, Bi. Fadhila Saidi (kulia), akiwa pamoja na Mwenyekiti wa Mtaa wa Majimaji, Wilaya ya Masasi, Bw. Bakari Issa (kushoto), wakikata utepe kuashiria uzinduzi rasmi wa mnara wa 5G wa Yas katika Wilaya ya Masasi, Mkoa wa Mtwara, hivi karibuni. Teknolojia hiyo inatarajiwa kuboresha huduma za intaneti ya kasi, kuchochea ukuaji wa biashara na kuongeza upatikanaji wa huduma za kidijitali kwa wakazi wa Masasi na maeneo ya jirani.


NA: MWANDISHI WETU, PANGANI

Viongozi na watendaji wa matawi wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM), wilaya ya Pangani mkoani Tanga, wamepatiwa mafunzo ya kuwajengea uwezo wa masuala mbalimbali ya kichama, kiuongozi na kijamii ili kuboresha utendajikazi wao wa kila siku.

Mafunzo hayo yametolewa Agosti 2, 2026, katika Kata ya Kipumbwi wilayani humo.

Akizungumza katika mafunzo hayo, Mwenyekiti wa Seneti ya vyuo vya kati, vyuo na vyuo vikuu mkoa wa Tanga, Leila Mnaki, ambaye alikuwa miongozo mwa wakufunzi, amesema CCM ni Chama imara kwani misingi yake ipo ngazi za chini za mabalozi na matawi, hivyo ni wajibu wa Chama kutoa mafunzo ya mara kwa mara kwa viongozi wake ili kuboresha utendajikazi.

"Nguvu ya Chama ni wanachama na viongozi wake, ndiyo maana tupo hapa kupata mafunzo ya kutujengea uwezo ili utendajikazi wetu uwe wenye tija kwa manufaa ya Chama na wananchi tunaowahudumia," amesema Mnaki.

Aidha, Mnaki amesema, ni wajibu wa viongozi kuwahudumia wananchi kwa kufuata misingi ya Chama, ambayo imesisitiza kutanguliza maslahi ya wananchi ili kukuza maendeleo.

"Chama chetu hakiongozwi kwa utashi wa mtu, bali kanuni, miongozo na taratibu, ni matumaini yangu kuwa viongozi na watendaji mtazingatia hili katika Utumishi wenu wote," ameongeza.

Awali, mratibu wa mafunzo hayo, ambaye pia ni Katibu wa UVCCM wilaya, Nasri Mkalipa, aliwasisitiza viongozi hao kuzingatia yote na kuyatendea kazi.

"Niwasihi sana tuzingatie yote tutakayofundishwa hapa, kwani mafunzo haya ni mahsusi katika kuboresha utendajikazi wetu na kuonyesha utofauti wa kiuongozi," amesema Mkalipa.

Katika mafunzo hayo, mada mbalimbali zilifundishwa kwa viongozi hao. Miongoni mwa mada hizo ni pamoja na itikadi, kanuni na falsafa ya CCM, uandishi wa muhtasari na utunzaji kumbukumbu.

Pia, masuala ya uongozi wa kimkakati, ukatili wa kijinsia, afya ya akili, usalama barabarani na matumizi ya mitandao ya kijamii.

Ikumbukwe kuwa, mafunzo hayo maalum yamepewa jina la "Darasa la Ushindi" huku yakichagizwa na kaulimbiu ya "T3 - Tujifunze, Tuongoze na Tuwajibike".

Kimsingi, mkakati uliopo ni kufikisha mafunzo hayo katika kata zote 14 za wilaya hiyo, huku walengwa wa mafunzo hayo wakiwa ni wenyeviti, makatibu na makatibu hamasa wa UVCCM wa matawi yote wilayani humo.







Na Janeth Raphael - MichuziTv.

Serikali imesisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano kati ya sekta za kilimo, mifugo, uvuvi, viwanda, biashara na taasisi za kifedha ili kuongeza uzalishaji, kuimarisha uchakataji wa mazao na kuchochea ukuaji wa uchumi wa Taifa.

Msisitizo huo umetolewa leo Agosti 2, 2026 jijini Dodoma na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar, alipofanya ziara katika Viwanja vya Dk. John Samwel Malecela, Nzuguni, kujionea shughuli mbalimbali zinazoendelea katika Maonesho ya 33 ya Kimataifa ya Kilimo (Nanenane).

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Balozi Omar amesema maendeleo ya uchumi hayawezi kufikiwa kwa ufanisi ikiwa kila sekta itafanya kazi kwa kujitegemea, akieleza kuwa ushirikiano wa karibu kati ya sekta hizo ni msingi wa kuongeza tija, kuvutia uwekezaji na kuinua kipato cha wananchi.

Amesema Serikali inalenga kuona uzalishaji unaongezeka sambamba na kuongeza thamani ya mazao kupitia uchakataji, huku taasisi za kifedha zikiendelea kuwezesha maeneo yenye kipaumbele ili kuharakisha maendeleo ya sekta za uzalishaji.

"Ni muhimu kuwa na mtazamo wa pamoja wa kukuza uzalishaji, kuongeza thamani ya mazao kupitia uchakataji na kuhakikisha sekta zote zinashirikiana kwa manufaa ya wananchi na uchumi wa Taifa. Taasisi za kifedha zinapaswa kuendelea kuunga mkono maeneo ambayo Serikali imeyapa kipaumbele ili kuongeza kasi ya uwekezaji," amesema.

Katika hatua nyingine, Waziri huyo amesema Serikali inaendelea kufuatilia matumizi ya matrekta yaliyotolewa kwa wakulima ili kuhakikisha yanatumika katika maeneo yaliyokusudiwa na kuchangia kuongeza tija katika uzalishaji wa kilimo.

Aidha, amewapongeza wajasiriamali wanaozalisha bidhaa zenye ubora, huku akisisitiza umuhimu wa kuweka mikakati madhubuti ya kutafuta masoko ya ndani na nje ya nchi ili kuongeza ushindani wa bidhaa zinazozalishwa Tanzania.

Ameongeza kuwa pamoja na kuongeza uzalishaji, kuna haja ya kuwekeza zaidi katika utangazaji wa bidhaa, kuimarisha mifumo ya masoko na kuboresha mazingira ya biashara ili bidhaa za Kitanzania zipate nafasi kubwa katika masoko ya kikanda na kimataifa.





Chama Kikuu cha Ushirika Tandahimba na Newala (TANECU) kimetangaza mafanikio makubwa katika sekta ya korosho baada ya kufanikiwa kupata zaidi ya Sh bilioni 1.6 kupitia mauzo ya korosho kimataifa zilizoongezwa thamani katika kiwanda chake cha kubangua korosho, huku kikieleza kuwa kipo katika hatua za mwisho za kuanza ujenzi wa kiwanda cha pili Wilaya ya Tandahimba.

Akizungumza na waandishi wa habari kwenye Maonesho ya Kilimo Kitaifa Nanenane yanayoendelea Jijini Dodoma Agosti 2, 2026, Mwenyekiti wa TANECU, Karimu Hamis Chipola, alisema wamefika kwenye maonesho hayo kuonesha mafanikio ya wakulima na mchango wa ushirika katika kuongeza thamani ya mazao na kuwanufaisha wanaushirika.

Chipola alimshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuwaunganisha wakulima kupitia maonesho ya Nanenane, akisema yamekuwa jukwaa muhimu la kuonesha ubunifu na mafanikio ya sekta ya kilimo nchini.

Alisema TANECU imefanikiwa kutekeleza kwa kiwango kikubwa maelekezo ya Serikali ya Awamu ya Sita ya kuhakikisha ifikapo mwaka 2030 mazao yanayozalishwa nchini yanachakatwa na kuongezwa thamani ili kuongeza kipato cha wakulima.

“Tayari kiwanda chetu cha kubangua korosho kinafanya kazi na bidhaa zilizochakatwa zimeuzwa katika masoko ya kimataifa, ambapo tumepata zaidi ya shilingi bilioni 1.6. Hii ni hatua kubwa kwa wakulima wetu,” alisema Chipola.

Aliongeza kuwa maandalizi ya ujenzi wa kiwanda cha pili yamefikia hatua ya mwisho ya manunuzi, hatua ambayo itaongeza uwezo wa kuchakata korosho na kupanua masoko ya bidhaa za wakulima.

Katika kuboresha mfumo wa biashara ya korosho, Chipola alisema TANECU inaendelea kutekeleza maelekezo ya Wizara ya Kilimo kuhusu uuzaji wa korosho ghafi kupitia mfumo wa stakabadhi za ghala na Soko la Bidhaa Tanzania.

Pia alisema baada ya ziara ya Waziri wa Kilimo, Daniel Chongolo, mkoani Mtwara, TANECU ilielekezwa kujenga maghala ya kuhifadhi korosho ili kupunguza gharama za usafirishaji kwa wakulima.

Kwa mujibu wa Chipola, wamepanga kujenga maghala sita, ambapo mawili tayari yamekamilika na yanatarajiwa kuzinduliwa Septemba 1, 2026, kabla ya kuanza kutumika katika msimu mpya wa mauzo ya korosho. Maghala manne yaliyobaki yataendelea kujengwa ili kukamilisha mpango huo.

Akizungumzia jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita, Chipola alisema serikali imeendelea kuwainua wakulima kupitia ruzuku ya pembejeo yenye thamani ya zaidi ya Sh trilioni 1.1.

Alisema TANECU imeunga mkono juhudi hizo kwa kuajiri maafisa ugani 13 waliopangiwa kufanya kazi katika wilaya za Tandahimba na Newala, ambapo wanatoa elimu ya matumizi sahihi ya pembejeo na mbinu bora za kilimo ili kuongeza uzalishaji.

Aidha, TANECU imejipanga kuendeleza kampeni ya “Linda Ushirika, Chagua Uadilifu”, iliyoanzishwa na Tume ya Maendeleo ya Ushirika kwa kushirikiana na Wizara ya Kilimo, kwa kuendelea kutoa elimu kwa wakulima kuhusu umuhimu wa kulinda ushirika na kusimamia uwajibikaji.

Aliwahimiza wananchi wanaotembelea Maonesho ya Nanenane Jijini Dodoma kufika katika banda la TANECU kujionea bidhaa mbalimbali zinazozalishwa na ushirika huo, hususan korosho zilizoongezwa thamani, pamoja na kupata elimu kuhusu kilimo na ushirika.





Na Janeth Raphael – Michuzi TV

Watu wanane wamefariki dunia na wengine 66 kujeruhiwa kufuatia ajali mbaya iliyohusisha mabasi mawili ya abiria yaliyogongana uso kwa uso katika eneo la Ibihwa, Halmashauri ya Wilaya ya Bahi, mkoani Dodoma.

Kaimu Kamanda wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, Rehema Jeremia, amethibitisha kutokea kwa ajali hiyo, akieleza kuwa ilihusisha basi la Isamilo lenye namba za usajili T 428 EXP, lililokuwa likitoka Mwanza kuelekea Dar es Salaam, na basi la Libanika Luxury lenye namba za usajili T 897 DUP, lililokuwa likitoka Dar es Salaam kuelekea Mwanza.

Akizungumza baada ya kuwatembelea majeruhi waliolazwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule, amesema watu saba walifariki dunia papo hapo eneo la tukio, huku mtu mmoja akifariki baadaye alipokuwa akipatiwa matibabu hospitalini, na kufanya idadi ya vifo kufikia wanane.

Senyamule amesema kati ya majeruhi 66, watu tisa wanaendelea kupatiwa matibabu wakiwa katika hali mbaya, huku majeruhi 57 wakiwa katika hali ya kuridhisha.

Ameongeza kuwa majeruhi wamepelekwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma, Hospitali ya Makole na Hospitali ya Wilaya ya Bahi, ambako wanaendelea kupatiwa huduma za matibabu.

Kwa mujibu wa uchunguzi wa awali, chanzo cha ajali hiyo kinadaiwa kuwa ni dereva mmoja kujaribu kulipita gari lingine bila kuchukua tahadhari stahiki, hali iliyosababisha mabasi hayo kugongana uso kwa uso.

Mmoja wa majeruhi wa ajali hiyo, Jail Martin, amesema tukio hilo lilitokea majira ya saa 12:00 asubuhi baada ya basi walilokuwa wakisafiria kuanza kuyumba kabla ya kugongana uso kwa uso na basi lililokuwa likitokea upande wa pili wa barabara.

Jeshi la Polisi pamoja na vyombo vingine vya uokoaji vinaendelea na uchunguzi wa kina kubaini chanzo halisi cha ajali hiyo huku juhudi za kuwahudumia majeruhi zikiendelea.





Na Mwandishi Wetu

MJUMBE wa Kamati ya Utekelezaji ya Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) Taifa, Mariam Abdallah Ibrahim ambaye pia ni Mbunge wa Mkoa wa Pwani ametoa Sh.milioni moja kwa ajili ya Kusaidia kukamilisha Ujenzi wa nyumba ya Mtumishi wa Jumuiya hiyo wilayani Gairo mkoani Pwani.


Mbunge Mariam amekabidhi fedha hizo akiwa katika ziara ya kutembelea na kukagua utekelezaji wa miradi ya maendeleo inayotekelezwa na vikundi vya wajasiriamali hasa walioko kwenye Jumuiya ya UWT .

Akiwa katika ziara hiyo alipata nafasi ya kukagua pia nyumba ya mtumishi wa Jumuiya ya UWT Wilaya ya Gairo ambapo amekabidhi mchango wake wq fedha Sh. milioni moja ili kusaidia kukamilisha ujenzi wa nyumba ya mtumishi huyo.

Akizungumza na wananchi na wanachama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) amewashukuru wakazi wa Mkoa wa Morogoro kwa kukichagua Chama Cha Mapinduzi katika Uchaguzi Mkuu kwa kumpatia kura nyingi Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na kuwachagua wabunge na madiwani wa chama hicho.

Mbunge Mariam pia amewahimiza wanawake kujitokeza kwa wingi kugombea nafasi za uongozi ndani ya CCM, akieleza kuwa ushiriki wao katika nafasi za maamuzi ni muhimu katika kuimarisha maendeleo na kuendelea kutetea maslahi ya wanawake na jamii kwa ujumla.

Ziara hiyo ni sehemu ya juhudi za UWT Taifa za kufuatilia utekelezaji wa shughuli za jumuiya hiyo, kuhamasisha maendeleo ya wanawake, na kuimarisha ushiriki wao katika shughuli za kisiasa, kijamii na kiuchumi.












Top News