Na Mwandishi Wetu

KATIKA kuunga mkono juhudi za Serikali za kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia, Oryx Gas Tanzania imetoa mafunzo ya matumizi salama na sahihi ya gesi ya kupikia kwa makundi ya wajasiriamali mbalimbali yakiwemo mama na baba lishe.

Mafunzo hayo yametolewa leo Julai 23,2026 katika Tamasha la Samaki Bagamoyo ambapo wajasiriamali zaidi ya 600 ambao wanashiriki tamasha hilo wamepatiwa mafunzo hayo kupitia maofisa wa Oryx Gas wakiongozwa na Meneja Mafunzo Peter Ndomba.

Akizungumza wakati wa mafunzo hayo Ndomba ametumia nafasi hiyo kuelezea amesema faida za kutumia LPG ikilinganishwa na nishati nyingine za kupikia, ikiwemo kupunguza gharama za uendeshaji, kuokoa muda wa kupika, kulinda afya kwa kupunguza moshi hatarishi, na kuhifadhi mazingira.

Pia amesema wajasiriamali na washiriki wa tamasha hilo wamejifunza mbinu bora za usalama zikiwemo ukaguzi wa mtungi, regulator na bomba kabla ya matumizi.

Nyingine ni namna ya kutambua uvujaji wa gesi na hatua sahihi za kuchukua,matumizi ya vifaa vilivyoidhinishwa na vyenye ubora,uhifadhi salama wa mitungi ya gesi, tahadhari za kuzuia ajali na hatua za kuchukua wakati wa dharura.

Aidha wamefundishwa mbinu bora za matumizi salama ya LPG katika shughuli za kila siku za upishi pamoja na athari za kuni na mkaa kwa mazingira na afya ya jamii hasa kwa kundi kubwa la wanawake ambao wanaathirika wa moshi wa kuni na mkaa kila siku.

“Kupitia mafunzo haya, Oryx Gas Tanzania inaendelea kuwawezesha wafanyabiashara wa chakula kutumia nishati safi kwa usalama, kuongeza ufanisi wa biashara zao na kuchangia afya bora pamoja na mazingira safi.

“Elimu ya matumizi salama ya LPG ni msingi wa kujenga jamii salama na kufanikisha ajenda ya taifa ya matumizi ya nishati safi ya kupikia.Oryx Gas Tanzania imekuwa kinara wa nishati safi na sasa imejikita pia kutoa elimu kwa makundi mchini Tanzaia ili kuhakikisha matumizi endelevu ya nishati safi.”










Serikali kupitia Mamlaka ya Udhibiti wa Nafaka na Mazao Mchanganyiko (COPRA) inaendelea kuimarisha uzalishaji na biashara ya zao la kitunguu kwa kukamilisha miongozo ya usimamizi wa zao hilo na kuendeleza miundombinu ya masoko, hatua zinazolenga kuongeza ushindani wa vitunguu vya Tanzania katika masoko ya kikanda na kimataifa.

Akizungumza wakati wa ziara yake ya kikazi Wilaya ya Karatu, Waziri wa Kilimo, Mhe. Daniel Chongolo (Mb), ameielekeza COPRA kukamilisha miongozo ya zao la kitunguu ndani ya miezi mitatu na kuanza mchakato wa kupanua Soko la Vitunguu la Endashangwet ili kuongeza fursa za masoko kwa wakulima.

Akipokea maelekezo hayo, Mkurugenzi Mkuu wa COPRA, Bi. Irene Mlola, amesema miongozo hiyo ipo katika hatua za mwisho kukamilishwa na itaweka mfumo rasmi wa biashara ya vitunguu kupitia matumizi ya vipimo sahihi, vifungashio sanifu na usimamizi bora wa masoko.

Katika mwaka 2025/2026, Tanzania ilisafirisha kilogramu *33,295,659* za vitunguu zenye thamani ya zaidi ya *Shilingi bilioni 1.9*. Kupitia hatua hizi, Serikali inalenga kuongeza thamani ya zao, kupanua masoko ya kimataifa na kuongeza kipato cha wakulima. 





-Agusia tamaa ya maisha inavyochochea biashara dawa za kulevya kwa vijana

-Ataka vyombo vya ulinzi na usalama kuchunguza wenye Show room 


Na Said Mwishehe,Michuzi TV

MKUU wa Wilaya ya Temeke mkoani Dar es Salaam Sixtus Mapunda, amesema njia madhubuti ya kumaliza biashara ya dawa za kulevya nchini ni kukata cheni yote ya biashara hiyo kuanzia katika ngazi ya jamii ya kwenye mitaa huku akiitaka wananchi kushiriki mapambano dhidi ya dawa za kulevya.

Mapunda ametoa kauli hiyo leo Julai 23,2026 alipokuwa mgeni rasmi katika Tamasha laKufikia na kuhamasisha jamii dhidi ya madhara ya dawa za kulevya lililoandaliwa na Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya(DCEA).

Amesema pamoja na juhudi za kudhibiti uzalishaji, usafirishaji na uhifadhi wa dawa za kulevya, hatua hiyo bado ni ngumu kutokana na mbinu mbalimbali zinazotumiwa na wahalifu, hivyo jamii inapaswa kuelekeza nguvu zaidi katika kuzuia matumizi ya dawa hizo.

"Siku tusipokuwa na watumiaji, maana yake tumeshakata cheni. Kwenye biashara yoyote demand ndiyo inaleta supply. Ukikata uhitaji, mzigo utakosa soko," amesema.

Amesema wazazi wana wajibu wa kuanza kuwapa watoto elimu kuhusu madhara ya dawa za kulevya tangu wanapoanza kupata ufahamu ili kuwajengea uwezo wa kukataa vishawishi vinavyoweza kuharibu maisha yao.

Aidha, amewatahadharisha vijana kutojaribu kutumia dawa za kulevya kwa kudhani ni fasheni au starehe, akieleza kuwa uraibu huanza taratibu lakini madhara yake huwa makubwa na wakati mwingine hushindikana kurekebishwa.

“Nilipotembelea banda la Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya nimeoneshwa sampuli mbalimbali za dawa za kulevya ambazo zimetengenezwa kama keki ambazo zinazotumiwa na baadhi ya wanafunzi wa sekondari na vyuo vikuu katika sherehe binafsi.

“Tumefika katika hatua mbaya huko nyuma tulianza kama watumiaji baadae tukawa watumiaji na wasafirishaji lakini hivi sasa tumekuwa watengenezaji wa dawa za kulevya.Ni hatua mbaya sana na hivyo niwajibu wetu kukomesha dawa hizo kwa wote kushiriki katika mapambano.”

Amefafanua iwapo baadhi ya wanafunzi wa sekondari na vyuoni wameanza kutumia dawa za kulevya je hilo Taifa mbele ya safari bila kuchukua hatua hatma ya nchi itakuaje.

Katika hatua nyingine, amevitaka vyombo vya ulinzi na usalama kuendelea kufuatilia mitandao inayohusishwa na biashara haramu ya dawa za kulevya pamoja na mifumo ya utakatishaji fedha, akisema baadhi ya maisha ya anasa yasiyoelezeka yanaweza kuwa yanawavutia vijana kuingia katika biashara hiyo.

Ametoa mfano katika mitandao ya kijamii kuna baadhi ya watu wanaweka video wakionesha fedha bila kueleza walikozitoa jambo ambalo linalotia shaka na walikozipata na wanafanya hivyo kama sehemu ya kuhamasisha vijana kuingia kwenye maisha ya Misheni Town.

“Nilishasema katika Wilaya ya Temeke ni marufu wananchi kuonesha fedha katika mitandao ya kijamii na nikibaini tu huyo aliyeonesha hiyo video atamakatwa akahojiwe alikotoa hizo fedha maana fedha iliyotafutwa kwa jasho huwezi kuonesha.

“Nilimkamata cha kwanza nitawaambia TRA wakate kodi yao na kisha Polisi wamuweke mahabusu kwa ajili ya usalama wake maana anakaribisha wezi mtaani kwake.Lakini nyuma ya hizi video kuna mazingira ya kuhamasisha vijana kuingia kwa lengo la kutafuta maisha rahisi na matokeo yake unaingizwa katika biashara haramu kama ya dawa za kulevya.”

Pia amesema kwasasa mtaani kumekuwepo na maeneo mengi ya kuuza magari tena yenye gharama kubwa akitoa mfano uwepo wa Show room maeneo ya Buza au Mbagala.”Unajiuliza nani anaweza kununua BMW Buza?

“Sio kwamba nawatuhumu hapana lakini inatia mashaka na vyombo vya ulinzi mnaweza kwenda kuzungumza nao kirafiki tu.Isije ikawa mtu anatumia biashara ya magari kutakatisha fedha ambazo zimetokana na dawa za kulevya.”

Pia amewataka wananchi kutoa taarifa kuhusu watu wanaojihusisha na biashara ya dawa za kulevya badala ya kuwaficha, akisisitiza kuwa vita dhidi ya dawa za kulevya itafanikiwa pale jamii itakapokataa biashara hiyo kwa vitendo na si kwa maneno pekee.

Pamoja na hayo amesema mapambano dhidi ya dawa za kulevya yanahitaji ushirikiano wa serikali, wazazi, vijana na jamii kwa ujumla ili kulinda kizazi cha sasa na cha baadaye dhidi ya athari za janga hilo.









Na Benny Mwaipaja, London.

Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), amewakaribisha wawekezaji kutoka jumuiya ya kimataifa, kuchangamia fursa za uwekezaji nchini Tanzania katika sekta mbalimbali zikiwemo miundombinu, nishati, viwanda, kilimo, madini na huduma za kifedha.

Mhe. Balozi Omar ametoa wito huo jijini London nchini Uingereza alipoongoza ujumbe wa Tanzania katika Mkutano wa Kimkakati wa Uwekezaji na Ushirikiano wa Tanzania (Tanzania Strategic Investment and Partnership Forum) ukiwakutanisha viongozi wakuu wa taasisi kubwa za kifedha duniani, sekta ya bima na vihatarishi ulioandaliwa na Wizara ya Fedha kwa kushirikiana na Standard Bank ya nchini humo.

Alisema kuwa Serikali imeweka mazingira bora ya uwekezaji pamoja na vivutio vya kikodi ili kuvutia mitaji kutoka nje itakayochangia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayoelekeza nchi ifikie uchumi wa dola za Marekani trilioni 1 ifikapo mwaka 2050 ambapo asilimia 70 ya fedha hizo zinatarajiwa kutoka sekta binafsi.

Awali, katika hotuba yake, Mhe. Balozi Omar aliwasilisha mwelekeo wa uchumi wa Tanzania chini ya Dira ya Maendeleo 2050, akibainisha kwamba uchumi wa Tanzania ulikua kwa asilimia 5.9 mwaka 2025, ukilinganisha na asilimia 5.5 mwaka 2024 huku Mfumko wa bei ukiendelea kubaki chini ya asilimia 5, miongoni mwa viwango vya chini zaidi barani Afrika;

Alisema kuwa nakisi ya bajeti imepungua hadi asilimia 3.1 ya Pato la Taifa; Karibu asilimia 74.2 ya bajeti ya Taifa sasa inagharamiwa na mapato ya ndani; Deni la Taifa linabaki himilivu kulingana na tathmini ya Shirika la Fedha la Kimataifa-IMF.

Kwa upande wao, Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa Standard Bank Ulaya na Mkurugenzi Mtendaji wa Standard Bank Tanzania, Bwana Ian Carson, alisisitiza dhamira ya benki hiyo ya kuendelea kuunganisha Afrika na masoko ya fedha ya kimataifa, akiitaja Tanzania kuwa miongoni mwa maeneo bora zaidi barani Afrika kwa uwekezaji wa muda mrefu.

Akizungumza wakati wa Mkutano huo, Balozi wa Tanzania nchini Uingereza, Mhe. Balozi Mbelwa Kairuki, alisema Serikali inaendelea kuwa na dhamira ya kudumisha mazungumzo ya mara kwa mara na jumuiya ya kimataifa ya wawekezaji.

"Tanzania inatekeleza mpango kabambe wa mageuzi ya kiuchumi unaojikita katika usimamizi imara wa uchumi mkubwa, mageuzi ya kimuundo na ushiriki wa sekta binafsi. Tunakaribisha ushirikiano endelevu na wawekezaji wa kimataifa kama washirika katika kufikia ukuaji wa uchumi endelevu na jumuishi," alisema Mhe. Balozi Kairuki.

Wawekezaji kadhaa walitaka ufafanuzi kuhusu mradi wa dola bilioni 42 wa Gesi Asilia Iliyogandamizwa (LNG) ambapo Mhe. Balozi Omar alieleza kuwa mazungumzo yamepiga hatua kubwa na masuala yaliyobaki ni ya ndani kati ya washirika wa kibiashara, huku Serikali ikiwa tayari kuendelea mara washirika hao watakapokamilisha michakato yao ya ndani.

Aidha, wawekezaji walionesha shauku kubwa kuhusu Reli ya Kisasa (SGR), Bandari za Dar es Salaam, Tanga na Mtwara, pamoja na njia za kibiashara za kikanda ambapo Serikali ilieleza kuwa ifikapo 2030/31, karibu kilomita zote 2,000 za mtandao wa SGR zitakuwa zimekamilika, hatua itakayoimarisha nafasi ya Tanzania kama lango kuu la kibiashara Afrika Mashariki.

Masuala mengine yaliyojadiliwa ni pamoja na upatikanaji wa fedha za kigeni, usalama wa nishati, uchumi wa kidijitali, kilimo na uongezaji thamani wa mazao kama pamba (mpango wa "Cotton-to-Cloth").

Mkutano huo, ambao ni sehemu ya jitihada endelevu za kidiplomasia za kiuchumi za Tanzania, uliongozwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Hamis Mussa Omar (Mb), akiambatana na Kamishna wa Usimamizi wa Deni la Serikali, Bwana Japhet Justine, huku Ubalozi wa Tanzania nchini Uingereza ukiwakilishwa na Mhe. Balozi Mbelwa Kairuki.


Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akizungumza wakati wa Mkutano wa Kimkakati wa Uwekezaji na Ushirikiano wa Tanzania (Tanzania Strategic Investment and Partnership Forum) uliowakutanisha viongozi wakuu wa taasisi kubwa za kifedha duniani, sekta ya bima na vihatarishi, ulioandaliwa na Wizara ya Fedha kwa kushirikiana na Standard Bank, Jijini London nchini Uingereza.

(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini-Wizara ya Fedha-London).








Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amezindua rasmi huduma za usafiri wa umma kwa kutumia mabasi ya umeme pamoja na Kituo cha Mabasi Malindi leo, tarehe 23 Julai 2026.

Katika hafla hiyo, Rais Dkt. Mwinyi ameitaka ZSSF kukamilisha kwa haraka ujenzi wa vituo vya kisasa vya mabasi ili wananchi wanufaike kikamilifu na huduma hiyo. Amesema mradi wa mabasi ya umeme utaboresha usafiri wa umma, kupunguza uchafuzi wa mazingira na kuongeza matumizi ya nishati safi.

Halikadhalika, Rais Dkt. Mwinyi  amesisitiza kuwa Serikali itaendelea kutekeleza miradi mikubwa ya maendeleo ikiwemo barabara, maji, bandari, viwanja vya ndege, hospitali na Mji wa Michezo unaojiandaa kuhudumia mashindano ya AFCON, huku akiwataka wananchi kuilinda miundombinu ya umma na kuendelea kuunga mkono juhudi za maendeleo.

Hafla hiyo pia ilihusisha uzinduzi wa kadi maalumu za usafiri kwa wanafunzi, wazee na abiria wengine, hatua inayolenga kuboresha upatikanaji wa huduma za usafiri kwa makundi mbalimbali ya wananchi.












Wananchi wa Kata ya Chang'ombe na Totowe, Wilaya Songwe Mkoa wa Songwe, wametakiwa kuendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi katika  kupambana na uhalifu, hususan vitendo vya ukatili dhidi ya watoto, kwa kutoa taarifa za uhalifu na wahalifu ili hatua za kisheria zichukuliwe kwa wakati.

Kauli hiyo ilitolewa na Mkuu wa Mkoa wa Songwe, Mh. Jabiri Makame, Julai 22, 2026, wakati wa ziara kampeni  inayoitwa kwa  jina la Serikali Nyumbani Kwako, ambapo alisisitiza kuwa vitendo vya ukatili dhidi ya watoto havikubaliki, huku akieleza kuwa ni wajibu wa kila mwananchi kuwalinda, kuwatunza na kuwalea watoto kwa upendo kwa kuwa ndiyo msingi wa taifa la kesho.

Akizungumza katika ziara hiyo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Songwe, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Augustino Senga, aliwataka wananchi kupiga vita matukio ya ubakaji na ulawiti katika  maeneo yote, hivyo kila mwananchi ana wajibu wa kulinda watoto wa kike na wa kiume pamoja na kuheshimu haki na usalama wa watu wote katika jamii.

Aidha Kamanda Senga aliwasisitiza wananchi  kupambana dhidi ya makosa hayo maana yanahitaji ushirikiano wa wananchi  na Jeshi la Polisi katika kutoa taarifa za uhalifu kwa kuyazuia matukio hayo kabisa katika jamii.

Pia Kamanda Senga aliwataka wananchi kuachana na matumizi mabaya ya fedha kwa mambo yasiyo na tija na badala yake kuelekeza rasilimali katika kuboresha maisha ya familia, malezi ya watoto na shughuli za maendeleo. 

Mwisho, Kamanda Senga alimalizia kwa kutoa wito kwa wananchi wote kuendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi katika kuzuia na kupambana na uhalifu, akieleza kuwa ushirikiano huo utasaidia kukomesha ubakaji, ulawiti, ulevi wa kupindukia na vitendo vingine vya kihalifu ili kujenga jamii salama, yenye amani na inayowalinda watoto. 









 


Na. Mwandishi wetu Jeshi la Polisi

NDOTO za vijana wanaoishi katika mazingira magumu mkoani Arusha zimeanza kupata mwanga baada ya Jeshi la Polisi Kikosi cha Usalama Barabarani mkoani humo, kuzindua mpango wa kuwabaini na kuwapa mafunzo ya udereva bila malipo kwa kushrikiana na vyuo vya udereva, hatua inayolenga kuwajengea ujuzi na kuwainua kiuchumi.

Akizungumza mara baada ya kufungua mafunzo hayo leo, Mkuu wa Kikosi cha Usalama barabarani mkoani humo, ACP Zauda Mohamed amesema mpango huo ni sehemu ya mkakati wa kuwawezesha vijana, ili kuwaondoa kwenye mazingira magumu yanayoweza kuwashawishi kujihusisha na vitendo vya kihalifu kwa kuwapatia ujuzi utakaowajengea uwezo wa kujitegemea.

ACP Zauda amebainisha kuwa, vijana hao waliwachukua kutoka sehemu mbalimbali ikiwemo vituo vya kulelea watoto wenye changamoto za malezi, maeneo ya kuegesha na kuosha magari, wanaobeba mizigo sokoni pamoja na wapiga debe katika vituo vya mabasi.

Aidha, amefafanua kuwa pamoja na kugharamia mafunzo hayo, Jeshi hilo pia litahakikisha linawasimamia vijana hao katika hatua zote za kupata leseni za udereva ili kuongeza fursa zao za kujiajiri au kuajiriwa mara baada ya kuhitimu mafunzo.

Mkuu huyo wa usalama barabarani amemaliza kwa kusema kuwa, anaamini kuwa baada ya vijana hao kuhitimu na kupata leseni zao za udereva, itakuwa ni chachu ya mabadiliko kwao kiuchumi, kuwaondoa katika makundi hatarishi lakini poa kuwaepusha na uhalifu.

Naye Bw. Godfrey Laizer, mnufaika wa mafunzo hayo anayejishughulisha na kubeba mizigo amesema mafunzo hayo yamempa matumaini mapya, akieleza kuwa yatamwezesha kupata leseni ya udereva na kufungua fursa za ajira pamoja na kuboresha maisha yake.

Kijana kutoka kituo cha kulelea watoto yatima cha Kindness Children Care, Bw. Steven Daniel amelishukuru Jeshi la Polisi kwa fursa hiyo, akisema watajituma katika mafunzo ili kutimiza ndoto zao za badaye.

Kwa upande wake Bi. Emmy Frank anayejishughulisha na kuosha magari amesema mafunzo hayo yatamjengea ujuzi na kumpa nafasi ya kupata ajira zenye kipato bora. Ameahidi kuitumia vyema fursa hiyo na kuzingatia mafunzo yote atakayopatiwa.


SERIKALI imeagiza Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea Tanzania (TFRA) kuhakikisha inasimamja usambazaji wa mbolea kwa wakulima nchini wakiwemo wakulima wa kijiji cha Mang’ola, Wilaya ya Karatu Mkoani Arusha.

Amesema Waziri wa Kilimo, Mhe. Daniel Chongolo (Mb) akiwa katika ziara ya kikazi mkoani humo tarehe 22 Julai 2026 ili kukagua miradi ya maendeleo.

“Niwapomgeze wananchi wa Mang’oa kwa kujishughulisha na kilimo cha vitunguu na mazao memgime. Nimeielekeza TFRA na Kampuni ya Mbolea Tanzania (TFC) kuhakikisha mbolea inayosambazwa nchini inawafikia,” amesema Waziri Chongolo.

Aidha, Mkurugenzi Mkuu wa TFC, Bw. Samwel Mshote amesema kuwa tani elfu mbili za mbolea ya DAP zinapelekwa ndani ya wiki mbili katika kijiji hicho huku taratibu za kuwa na myrndaji wa TFC kuwepo Mang’oa zitatekelezwa ili wakulima wapatiwe elimu ya matumizi sahihi ya mbolea.

Sambamba na hilo, Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea Tanzania (TFRA) Joel Lauren amesema kuwa wakulima wataendelea kupatiwa mafunzo ya matumizi sahihi ya mbolea kupitia Kampeni ya Mali Shambani inayoratibiwa na Wizara ya Kilimo kuanzia mwezi Agosti 2026 .

Ameeleza kuwa “matumizi mbadala si kununua mbolea kwa jina badala yake ni kuwa na elimu ya sahihi ya matumizi ya mbolea kwa kuendana na virutubisho, afya ya udongo na mbegu bora.”

Kuhusu biashara holela ya mbolea, Bw. Laurent amesema kuwa hakuna mfanyabiashara atakayeruhusiwa kuuza mbolea kinyume na masharti ya leseni yake na moja ya adhabu ni kufutiwa leseni. Mpango wa ruzuku bado upo kupitia maelekezo ya Serikali ambayo imetoa fedha kuhakikisha mkulima anapata bei himilivu ya mbolea.




















Top News