Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Deogratius Ndejembi, ameagiza Mamlaka na Taasisi zinazohusika kuchukua hatua za haraka kujiandaa ili kuzuia na kupunguza athari zinazoweza kusababishwa na mvua za El Niño zinazotarajiwa kuanza mwezi Oktoba 2026.

Makamu wa Rais ametoa maagizo hayo, mara baada ya kupokea taarifa ya utayari na maandalizi ya Serikali kufuatia tahadhari iliyotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania kuhusu mvua za El- nino, katika kikao kilichofanyika Ofisi ya Makamu wa Rais Jijini Dar es Salaam.

Akizungumza na Viongozi pamoja na timu ya wataalamu kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Wizara ya Ujenzi pamoja na Taasisi zilizochini ya Wizara hizo, Makamu wa Rais amesisitiza umuhimu wa taasisi zote zinazohusika, kufanya kazi kwa pamoja na kuchukua hatua za tahadhari mapema ili kuzuia au kupunguza athari zinazoweza kutokea kwa wananchi kufuatia ujio wa mvua hizo.

Pia amesisitiza umuhimu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama kushirikishwa katika maandalizi hayo ili kuwa na nguvu kazi ya kutosha pamoja na kuimarisha uwezo wa Serikali wa kuzuia, kupunguza na kukabiliana kwa haraka na athari zinazoweza kujitokeza.

“Ifanyike kampeni ya haraka, mikondo na mifereji ya maji izibuliwe, na barabara ziandaliwe,” amesisitiza Makamu wa Rais.

Aidha, ameelekeza taka, tope na udongo unaotolewa baada ya kuzibua mitaro na mifereji katika maeneo mbalimbali kuondolewa mara moja na kutupwa katika maeneo yaliyotengwa, badala ya kuachwa kandokando ya barabara ambako unaweza kurejea kwenye mifereji wakati mvua zinapoanza.

Makamu wa Rais pia ameagiza mamlaka husika kuwasimamia wakandarasi wanaotekeleza miradi ya ujenzi wa barabara, kuchukua hatua za haraka kusambaza vifusi vilivyorundikwa katika maeneo yenye shughuli za ujenzi, akisisitiza kuwa kazi hiyo haipaswi kusubiri hadi mvua zianze kunyesha kwani husababisha usumbufu na kero kwa wananchi.

Amesema katika maeneo yenye miradi ya ujenzi wa barabara ni lazima kuwe na mipango madhubuti itakayohakikisha barabara zinaendelea kupitika kwa urahisi na usalama, ili shughuli za ujenzi zisigeuke kuwa chanzo cha usumbufu au kuongeza athari kwa wananchi wakati wa mvua.

Katika kikao hicho, Makamu wa Rais alipokea taarifa kutoka kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, Mhe. Mhandisi Hamad Yusuf Masauni; Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Prof. Riziki Shemdoe; pamoja na Naibu Waziri wa Ujenzi, Mhandisi Godfrey Kasekenya.

Taarifa ziliyowasilishwa katika kikao hicho zimeeleza kuwa maandalizi yanaendelea vizuri kupitia Kamati ya Kitaifa iliyoundwa kuratibu hatua za kuzuia, kudhibiti na kukabiliana na majanga yanayoweza kujitokeza katika kipindi cha mvua za El Niño.

Miongoni mwa maeneo yaliyopewa kipaumbele ni kufanya tathmini ya makazi yaliyopo mabondeni na maeneo mengine yenye hatari ya mafuriko, kuongeza elimu na tahadhari kwa umma, kufanya tathmini ya masoko na maeneo yenye mikusanyiko mikubwa ya watu, pamoja na kuendesha kampeni za usafi wa mazingira.

Hatua nyingine ni kuzibua mitaro, mifereji na mikondo ya maji, kulinda njia za asili za maji, kudhibiti maji taka na kufanya ukaguzi wa madaraja pamoja na miundombinu mingine muhimu ili kubaini maeneo yenye hatari na kuchukua hatua kabla ya mvua kuanza.

Serikali pia imeweka mkazo katika kuwa na mpango shirikishi wa dharura utakaowezesha Taasisi mbalimbali kuratibu hatua za uokoaji na utoaji wa huduma muhimu endapo kutatokea mafuriko au majanga mengine yanayohusiana na mvua hizo.







Na. Peter Haule, WF, Nairobi, Kenya

Tanzania na Marekani zimeeleza dhamira ya kuendelea kuimarisha ushirikiano katika sekta mbalimbali za maendeleo, ikiwemo afya, kilimo, nishati, madini, miundombinu, elimu na utalii.

Dhamira hiyo imeelezwa wakati Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula (Mb), alipokutana na kufanya mazungumzo na Naibu Katibu wa Hazina ya Marekani anayeshughulikia Masuala ya Kimataifa, Bi. Erin Browne, mjini Nairobi, Kenya, kando ya Jukwaa la Mazungumzo ya Ngazi za Juu la Mawaziri wa Fedha kuhusu kuimarisha uwekezaji wa pamoja katika sekta ya afya.

Katika mazungumzo hayo, Mhe. Luswetula amezialika kampuni na wawekezaji kutoka Marekani kutumia fursa mbalimbali za uwekezaji zinazopatikana Tanzania, akitaja maeneo ya kilimo, nishati, madini, miundombinu, afya, elimu na utalii.

Aidha, Mhe. Luswetula ameishukuru Serikali ya Marekani kwa kuendelea kushirikiana na Tanzania pamoja na mchango wake katika maeneo mbalimbali ya maendeleo tangu kuanzishwa kwa uhusiano wa kidiplomasia kati ya nchi hizo mwaka 1968.

Amesema ushirikiano huo umekuwa na mchango katika juhudi za Tanzania za kukuza maendeleo ya kijamii na kiuchumi na kupunguza umaskini.

Kwa upande wake, Naibu Katibu wa Hazina ya Marekani anayeshughulikia Masuala ya Kimataifa, Bi. Erin Browne, amesema Marekani itaendelea kushirikiana na Tanzania katika maeneo mbalimbali ya maendeleo, pamoja na kuimarisha na kukuza ushirikiano uliopo baina ya nchi hizo.

Mazungumzo hayo yameangazia pia umuhimu wa kuendelea kujenga ushirikiano wa kiuchumi na uwekezaji kati ya Tanzania na Marekani kwa manufaa ya wananchi wa nchi hizo mbili.
Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula (Mb) akisalimiana na Naibu Katibu wa Hazina ya Marekani anayeshughulikia Masuala ya Kimataifa, Bi. Erin Browne, mjini Nairobi, Kenya, kando ya Jukwaa la Mazungumzo ya Ngazi za Juu la Mawaziri wa Fedha kuhusu kuimarisha uwekezaji wa pamoja katika sekta ya afya.



Naibu Katibu wa Hazina ya Marekani anayeshughulikia Masuala ya Kimataifa, Bi. Erin Browne, mjini Nairobi, Kenya, akizungumza kuhusu ushirikiano wa maendeleo wakati wa mkutano na Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula (Mb), kando ya Jukwaa la Mazungumzo ya Ngazi za Juu la Mawaziri wa Fedha kuhusu kuimarisha uwekezaji wa pamoja katika sekta ya afya.




Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula (Mb) (katikati), akieleza fursa za uwekezaji wakati wa mkutano na Naibu Katibu wa Hazina ya Marekani anayeshughulikia Masuala ya Kimataifa, Bi. Erin Browne kando ya Jukwaa la Mazungumzo ya Ngazi za Juu la Mawaziri wa Fedha Afrika, kuhusu kuimarisha uwekezaji wa pamoja katika sekta ya afya, wengine ni wajumbe walioambatana nae kutoka Tanzania.




Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula (Mb) (wa pili kushoto) na Naibu Katibu wa Hazina ya Marekani anayeshughulikia Masuala ya Kimataifa, Bi. Erin Browne (wa pili kulia) wakiwa katika mkutano kati yao, kando ya Jukwaa la Mazungumzo ya Ngazi za Juu la Mawaziri wa Fedha Afrika, kuhusu kuimarisha uwekezaji wa pamoja katika sekta ya afya.





Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula (Mb) na Naibu Katibu wa Hazina ya Marekani anayeshughulikia Masuala ya Kimataifa, Bi. Erin Browne wakiteta jambo, kando ya Jukwaa la Mazungumzo ya Ngazi za Juu la Mawaziri wa Fedha Afrika, kuhusu kuimarisha uwekezaji wa pamoja katika sekta ya afya.



(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Fedha)
Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Mheshimiwa Dkt. Rhimo Nyansaho (Mb), tarehe 10 Septemba 2026, amekutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Ulinzi na Uzalishaji wa Kijeshi na Amiri Jeshi Mkuu wa Jamhuri ya Kiarabu ya Misri, Mheshimiwa Luteni Jenerali Ashraf Salem Zaher, jijini El Alamein, Misri.

Mazungumzo hayo ya viongozi hao waandamizi yalilenga kujadili na kuimarisha maeneo mbalimbali ya ushirikiano baina ya Wizara za Ulinzi za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Jamhuri ya Kiarabu ya Misri, ambazo ni nchi rafiki zenye uhusiano wa muda mrefu na wa kihistoria.

Aidha, viongozi hao walijadili masuala mbalimbali ya kiulinzi na usalama, pamoja na utekelezaji wa mambo yaliyojadiliwa wakati wa ziara ya Rais wa Jamhuri ya Kiarabu ya Misri, Mheshimiwa Abdel Fattah el-Sisi, nchini Tanzania mnamo Julai 18, 2026, ambapo alifanya mazungumzo na mwenyeji wake, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Mazungumzo hayo yalisisitiza umuhimu wa kuendelea kuimarisha uhusiano na ushirikiano wa kiulinzi na kijeshi baina ya Tanzania na Misri, hususan katika maeneo yenye maslahi ya pamoja kwa manufaa ya mataifa hayo mawili.

Katika ziara yake nchini Misri, Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Mheshimiwa Dkt. Rhimo Nyansaho (Mb), pia alipata fursa ya kushiriki katika Maonesho ya Kimataifa ya Anga na Teknolojia za Anga za Juu ya El Alamein (EIAS), yanayofanyika jijini El Alamein, Misri.

Maonesho hayo yamewakutanisha viongozi waandamizi wa Serikali, Mawaziri wa Ulinzi, Wakuu wa Majeshi, viongozi wa mashirika na kampuni mbalimbali za kimataifa, wanazuoni pamoja na wataalamu kutoka sekta ya ulinzi na anga, kutoka zaidi ya nchi 60 duniani.

Ushiriki wa Tanzania katika maonesho hayo unaendelea kutoa fursa muhimu ya kubadilishana uzoefu, maarifa na teknolojia katika sekta ya ulinzi na anga, pamoja na kujenga na kuimarisha mahusiano ya kimkakati na wadau mbalimbali wa kimataifa katika maeneo yenye maslahi ya pamoja.







Na Jane Mwakyoma - Rukwa

MAMLAKA ya mawasiliano Tanzania (TCRA) imewakutanisha wadau mbalimbali mkoani Rukwa wakiwemo watoa huduma za mawasiliano ya simu, sekta ya usafiri, vyombo vya ulinzi na usalama pamoja na makundi mbalimbali ya kijamii, kwa lengo la kujadili namna ya kukabiliana na kutokomeza uhalifu wa mtandaoni unaoendelea kushika kasi mkoani humo.

Akifungua mkutano huo jana kwa niaba ya mkuu wa mkoa wa Rukwa mkuu wa wilaya ya Nkasi Peter Lijualikali amewataka wananchi kuendelea kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama kwa kutoa taarifa na kuripoti vitendo vya uhalifu wa mtandaoni, ikiwemo kuwabaini na kuwafichua wahalifu waliopo katika maeneo yao.

"Tushirikiane kwa pamoja katika kutokomeza uhalifu wa mitandaoni Rukwa bila matukio haya inawezekana nguvu ya pamoja inahitajika." Amesema Lijualikali.

kwa upande wake, mkurugenzi mkuu wa TCRA mhandisi Peter Mwasalyanda amesema bado kuna mwendelezo wa vitendo vya uhalifu vinavyofanyika kupitia huduma za simu na intaneti, huku mkoa wa Rukwa ukiendelea kukabiliwa na changamoto hiyo.

Amesema juhudi za kudhibiti vitendo hivyo zinahitaji ushirikiano wa karibu kati ya TCRA, vyombo vya ulinzi na usalama pamoja na jamii.

Akitoa takwimu mhandisi Mwasalyanda amesema mkoa wa Rukwa una jumla ya matukio 1330 kwa wilaya ya Sumbawanga, Kalambo 612, na wilaya ya Nkasi matukio 553.

Amesisitiza kuwa mafanikio katika kudhibiti uhalifu wa mtandaoni yanategemea ushirikiano wa wadau wote, kila mmoja akitimiza wajibu wake katika kuzuia na kupambana na vitendo hivyo.

Amesema TCRA itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali katika kutoa elimu na kuchukua hatua zinazolenga kuimarisha usalama wa watumiaji wa huduma za mawasiliano.

Aidha, wadau mbalimbali walioshiriki mkutano huo, wakiwemo viongozi wa dini, wamesisitiza umuhimu wa elimu, malezi bora na maadili mema katika jamii, hususan kwa watoto, ili kuwajengea uwezo wa kutambua na kujiepusha na vitendo vya uhalifu wa mtandaoni.

" Ni muhimu elimu ikatolewa kwa wananchi hasa waishio vijijini ili wawe na uelewa wa kutosha kwa kuwa wao ni wahanga wa matukio hayo " mmoja wa wadau amesema.









Kampuni ya mawasiliano ya Yas Tanzania imezindua minara miwili mipya ya 4G mkoani Kilimanjaro, ikiwa ni mwendelezo wa uwekezaji wake katika kupanua na kuboresha huduma za mawasiliano nchini.

Minara hiyo ambayo ipo katika wilaya ya Moshi Mjini na Mwanga inatarajiwa kuongeza uwezo na ubora wa mtandao, hususan huduma za intaneti, kwa wakazi, wafanyabiashara na taasisi katika maeneo hayo.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mkuu wa Yas - Kanda ya Kaskazini, Bw. Robert Sanyagi, alisema uwekezaji huo unatokana na ongezeko la mahitaji ya huduma za mawasiliano na matumizi ya huduma za kidijitali.

“Leo Watanzania wanahitaji zaidi ya huduma za kupiga simu. Wanahitaji intaneti yenye kasi na uhakika kwa ajili ya biashara, elimu, huduma za kifedha na shughuli nyingine za kila siku. Ndiyo maana tunaendelea kuwekeza katika teknolojia za 4G na 5G ili kuwafikia wananchi wengi zaidi,” alisema Sanyagi.

Alisema Yas itaendelea kupanua mtandao wake katika maeneo mbalimbali nchini, ikiwemo maeneo ya mijini na pembezoni, ili wananchi wanufaike na fursa zinazotokana na ukuaji wa uchumi wa kidijitali.

Akizindua mnara huo, mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Moshi ambaye ni Afisa Tarafa wa Moshi Mashariki, Bi. Khalima Idrisa, amesema mnara huo utaimarisha mawasiliano na kusaidia juhudi za Serikali katika kuboresha huduma hizo kwa wananchi.

Kwa upande wake, mkazi wa Kilimanjaro, Bi. Mwanaisha Juma, aliishukuru Yas na kusema kuwa kuimarika kwa huduma za mawasiliano kutapunguza changamoto ambazo wananchi walikuwa wakikumbana nazo hapo awali.

“Zamani tulikuwa tunapata changamoto kubwa sana za kimawasiliano, hasa kwenye huduma za kutuma na kupokea fedha. Wakati mwingine fedha zilikuwa zinachelewa kufika. Lakini sasa hivi hali imebadilika; huduma nyingi zinapatikana kwa urahisi kupitia mtandao. Tunaamini maboresho haya yataturahisishia zaidi maisha na shughuli zetu za kila siku,” alisema Bi.Mwanaisha.

Yas Tanzania imesema uzinduzi wa minara hiyo ni sehemu ya uwekezaji unaoendelea katika Kanda ya Kaskazini na maeneo mengine nchini, kwa lengo la kuwafikishia Watanzania huduma za mawasiliano zenye kasi na uhakika.




MAHAKAMA Kuu ya Tanzania imeamuru kutolewa kwa wito (summons) kwa Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP), Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi (CDF) na Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai (DCI), ili kutoa ushahidi katika kesi ya uhaini inayomkabili Mwenyekiti wa CHADEMA, Tundu Lissu.

Uamuzi huo umetolewa leo na jopo la majaji watatu wakiongozwa na Jaji Dustan Ndunguru baada ya Mahakama kusikiliza hoja za upande wa mashtaka na utetezi kuhusu ombi la Lissu la kuwaita mashahidi hao pamoja na viongozi wengine wa Serikali.

Mahakama imesema, kwa kuzingatia kifungu cha 314 cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai (CPA), ina hiari ya kuruhusu mashahidi kuitwa kwa kuangalia umuhimu wa ushahidi wao katika shauri.

Katika uamuzi huo, Mahakama imesema imeridhika kuwa ushahidi wa IGP, CDF na DCI ni muhimu katika kesi hiyo, hivyo imeamuru summons zitolewe ili waje kutoa ushahidi upande wa utetezi.

Hata hivyo, Mahakama imekataa ombi la kuwaita baadhi ya mashahidi waliotajwa na Lissu, akiwemo Rais Samia Suluhu Hassan na Waziri Mkuu wa zamani Kassim Majaliwa, ikisema ushahidi wao hauhusiani na kesi hiyo kwa upande wa utetezi.

Mahakama pia imekubaliana na hoja ya upande wa mashtaka kwamba mashahidi ambao hawakutajwa wakati wa committal proceedings hawawezi kutajwa baadaye wakati wa usikilizwaji wa hoja za awali (PH).

Jaji Ndunguru amesema kifungu cha 281 cha CPA kinaeleza kuwa msajili atatoa summons kwa mashahidi waliotajwa wakati wa committal proceedings, huku Mahakama ikibaini kuwa katika mwenendo wa kesi hiyo hakukuwa na orodha ya mashahidi waliotajwa.

Kuhusu hoja ya kumuita Mkurugenzi wa Usalama wa Taifa, Mahakama imesema mfano wa kesi ya Khatibu Ghandi hauwezi kutumika moja kwa moja kwa kuwa katika kesi hiyo shahidi huyo aliitwa na upande wa mashtaka na pia sheria ya sasa ya Usalama wa Taifa haikuwepo wakati huo.

Kesi hiyo imeahirishwa hadi kesho saa tatu asubuhi kwa ajili ya kuendelea na hatua ya utetezi.


Wadau wa kilimo-misitu nchini Tanzania wameanzisha jukwaa maalum (TASP), litakalowaunganisha wadau mbalimbali kwa ajili ya kubadilishana uzoefu, taarifa na ubunifu, pamoja na kuimarisha ushirikiano katika kuendeleza kilimo-misitu na kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi.

Akifungua jukwaa hilo Septemba 10, 2026 jijini Dodoma, Afisa Mazingira kutoka Wizara ya Kilimo, Nickson Kimaro, amesema kilimo-misitu ni agenda mtambuka inayohitaji ushirikiano wa Serikali, wakulima, taasisi za utafiti, sekta binafsi, asasi za kiraia, taasisi za fedha na washirika wa maendeleo.

Amesema TASP inapaswa kuwa mfumo endelevu wa uratibu utakaowezesha wadau kuoanisha jitihada zao, kubaini mapungufu na kutumia rasilimali kwa ufanisi, huku kilimo-misitu kikiwa na manufaa ya kiuchumi, kijamii na kimazingira.

Mkurugenzi Mtendaji wa Civic Social Protection Foundation (CPS), Nemence Iriya, amesema jukwaa hilo litatoa nafasi kwa wadau kukutana na kujadili sera, mikakati, sheria na taratibu zinazohusu kilimo-misitu, pamoja na kuimarisha uratibu wa shughuli zao.

Amesema TASP pia itasaidia kuhakikisha matokeo ya tafiti na ubunifu unaofanywa na watafiti unawafikia wakulima moja kwa moja, pamoja na watunga sera na wafanya maamuzi, na kuhalikisha tafiti hizo zinatumika katika kuboresha mipango na mikakati ya kilimo-misitu.

Kwa upande wake, Afisa Utafutaji Rasilimali Fedha, Mawasiliano na Utetezi kutoka VI-Agroforestry, Khalid Ngassa, amesema jukwaa hilo litawawezesha wadau kukutana pamoja, kubadilishana maarifa na uzoefu na kujadili changamoto zinazowakabili ili kupata suluhisho kwa pamoja.

Kwa ujumla, kuanzishwa kwa jukwaa hilo, kunatoa fursa muhimu ya kuwaunganisha wadau wa kilimo-misitu na kujenga mshikamano katika kushughulikia changamoto zinazowakabili, huku mafanikio ya jukwaa hilo yakitegemea utekelezaji wa mijadala na maazimio yaliyowekwa ili kuleta matokeo yanayoonekana kwa wakulima, kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi pamoja na maendeleo ya sekta hiyo nchini.














Na Nasra Ismail, Geita

Shirika la Arusha Society for the Protection of Animals (ASPA) kwa kushirikiana na Brooke East Africa limeendelea kutoa elimu kwa wafugaji na waendesha punda katika Kata ya Magenge, Halmashauri ya Wilaya ya Geita. Hii imechangia kuboresha ustawi wa mnyama kazi huyo katika maeneo hayo.

Kupitia elimu wanayopatiwa na mashirika hayo, wamiliki na waendesha punda wameanza kuona faida ya kumtunza mnyama huyo ambaye sasa ameanza kuwaingizia kipato tofauti na awali.

Wananchi wamesema sasa wana elimu ya kumtunza punda na namna sahihi ya kumfungia mkokoteni. Hii imesaidia kumpunguzia mnyama huyo vidonda na mateso, tofauti na kipindi kilichopita kabla ya kupata elimu hiyo.

Afisa Mifugo wa Kata ya Magenge, George Sebastianamesema kupitia elimu inayotolewa na ASPA, kwa kipindi kirefu sasa punda wameanza kuzaliana. Hii inaonesha kuwa punda sasa wanapata ustawi na wanaishi vizuri.

Kwa upande wake, Afisa Elimu ya Ustawi wa Wanyama kutoka ASPA, Diana Msemo amesema mnyama kazi punda anahitaji utulivu wa hali ya juu ili aweze kufanya kazi zake za kiasili na kuongeza uwezekano wa kupata ujauzito na kuongeza kizazi chake.

Msemo amebainisha baadhi ya mambo yanayompa utulivu mnyama huyo ni pamoja na kupata muda wa kupumzika, kupewa matibabu ya mara kwa mara na kupunguziwa mizigo ambayo haimudu.

 




MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA) imefanya Kikao Kazi cha Kwanza cha Jukwaa la Ushauri la Wadau wa TRA kuhusu Maadili, kinachofanyika mkoani Morogoro, kwa lengo la kuimarisha ushirikiano na wadau katika kukuza maadili katika usimamizi wa kodi na forodha.

Kikao hicho kimefanyika ikiwa ni utekelezaji wa ahadi iliyowekwa wakati wa uzinduzi wa Jukwaa hiloAprili 24, 2026, ambao ulikuwa mwanzo wa kujenga njia rasmi na endelevu ya kusikiliza maoni, changamoto na mapendekezo ya wadau kuhusu masuala ya maadili katika shughuli za TRA.

Akizungumza katika kikao hicho, Mkurugenzi wa Idara ya Mambo ya Ndani wa TRA, Shaibu Mmari, amesema maadili si suala la ndani ya TRA pekee, bali ni msingi muhimu wa kujenga uhusiano wa kuaminiana kati ya Mamlaka, walipakodi na jamii kwa ujumla.

Amesema ni muhimu walipakodi kutendewa kwa heshima, maamuzi kutolewa kwa misingi ya sheria na taratibu zinazoeleweka, pamoja na huduma kutolewa kwa wakati na kwa usawa, hatua ambazo zinaongeza imani ya walipakodi na kuimarisha ulipaji kodi kwa hiari.

Aidha, Mmari amewataka wajumbe wa Jukwaa hilo kuzungumza kwa uwazi na kutoa maoni kuhusu maeneo ambayo yanaweza kuwa na changamoto za kimaadili, ikiwemo ucheleweshaji wa huduma, matumizi mabaya ya mamlaka, changamoto katika mifumo ya kidijitali na njia za kutoa taarifa, huku akisisitiza umuhimu wa kutoa mapendekezo mahususi na yanayotekelezeka.

Kwa upande wake, Naibu Kadhi Mkuu, Sheikh Ali Khamis Ngeruko, amesema ni vyema watumishi wa TRA pamoja na walipakodi kuzingatia maadili katika kutekeleza majukumu yao ili kuhakikisha kodi zinalipwa kwa haki na kwa hiari. Aidha, amewataka watumishi na walipakodi kujiepusha na vitendo vya rushwa na kuzingatia uadilifu katika shughuli za kodi.

Kikao hicho kimewakutanisha wawakilishi kutoka vyama vya wafanyabiashara, walipakodi, washauri wa kodi, mawakala wa forodha, taasisi za Serikali, asasi za kiraia, taasisi za dini pamoja na viongozi na watendaji wa TRA, ambapo pamoja na kujadili masuala mbalimbali ya maadili, kikao hicho kinajadili pia rasimu ya Hadidu za Rejea za Jukwaa zitakazoweka msingi wa utekelezaji wa majukumu yake na ushirikiano endelevu na wadau.

 





Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, pamoja na Mawaziri, wakimfariji Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, nyumbani kwake Kizimkazi, Kusini Unguja, Zanzibar, tarehe 10 Septemba 2026, kufuatia kifo cha mume wake, Marehemu Maalim Hafidh Ameir Hassan, aliyefariki dunia tarehe 7 Septemba 2026.


















-Wananchi watakiwa kulinda daraja


‎Wananchi wa maeneo ya Chigongwe, Ngambala na Nguji kata ya Chigongwe wilayani Dodoma wameondokana na changamoto ya kukatika kwa mawasiliano wakati wa mvua baada ya kukamilika kwa ujenzi wa daraja la Chigongwe lenye urefu wa mita 36 katika barabara ya Chigongwe–Ngambala–Nguji.

‎Mradi huo umetekelezwa na Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) kupitia fedha za Mfuko wa Dharura (CERC) zilizotengwa kwa ajili ya kurejesha na kuboresha miundombinu iliyoathiriwa na mvua kubwa za mwaka 2024 hali iliyokuwa ikiathiri usafiri wa wananchi, usafirishaji wa mazao na upatikanaji wa huduma muhimu za kijamii.

‎Akizungumza wakati wa ukaguzi wa daraja hilo, Meneja wa TARURA wilaya ya Dodoma, Mhandisi Emmanuel Mfinanga amesema mradi huo uliogharimu shilingi milioni 606 umehusisha ujenzi wa daraja pamoja na uchongaji na uwekaji wa kifusi katika barabara kilomita 1 ambapo kwa sasa mradi umekamilika.

‎Mhandisi Mfinanga amewataka wananchi wanaotumia daraja hilo kulinda na kutunza ikiwemo kuzuia wizi wa vyuma vya ulinzi na kuepuka kufanya shughuli zinazoweza kuharibu daraja au kuzuia mtiririko wa maji.

‎Amesema ushirikiano wa wananchi katika kuitunza na kuilinda miundombinu ni muhimu ili kuhakikisha barabara, madaraja, makalavati na mifereji inaendelea kudumu kwa muda mrefu na kufanya kazi kwa ufanisi hususan wakati wa mvua kubwa.

‎Naye, Diwani wa kata ya Chigongwe Mhe. William Nado amesema ujenzi wa daraja hilo umeondoa changamoto iliyodumu kwa muda mrefu na kuwawezesha wananchi wa Mkombola na Ngambala kusafiri kwa urahisi wakati wote wa mwaka.

‎Amesema hapo awali mvua zilikuwa kikwazo cha usafiri ambapo wananchi walilazimika kuchangishana fedha na kurekebisha njia ili magari, pikipiki na watembea kwa miguu waweze kupita lakini sasa daraja hilo limeondoa kikwazo na wananchi wanasafiri bila shida.

‎Mhe. Nado amesema kukamilika kwa daraja hilo kumebadili hali ya usafiri kwani wananchi wanaweza kusafirisha mazao yao na mahitaji mengine kwa urahisi zaidi hasa kwa kutumia pikipiki na pia wanafunzi wanafika shuleni kwa urahisi.

‎Kwa upande wake, Mwenyekiti wa mtaa wa Ngambala Bw. Kenneth King’omah amesema daraja hilo limekuwa mkombozi kwa jamii hasa wajawazito, wazee na wagonjwa waliokuwa wakipata changamoto kufika katika vituo vya afya.

‎Amesema wananchi wamejipanga kushirikiana na TARURA na viongozi wa eneo hilo kuhakikisha daraja hilo linalindwa na kutunzwa ili liendelee kuwa kiungo muhimu cha huduma na shughuli za kiuchumi na kijamii.

‎Mkazi wa Ngambala na dereva wa bodaboda, Bw. Isaya Juma amesema ujenzi wa daraja hilo umeondoa adha kubwa iliyokuwa ikiwakabili waendesha pikipiki kwani awali walilazimika kushuka kwenye pikipiki na kupanda eneo hilo kwa shida wakati wa kuvusha abiria au mizigo jambo lililosababisha usumbufu na kuchelewesha safari.

‎Amesema kwa sasa hata ukiwa umepakia abiria watatu au wanne unapita bila shida ambapo ameishukuru serikali kwa daraja hilo kwasababu limeondoa changamoto iliyodumu kwa miaka mingi.













Top News