Na Mwandishi wa OTR

Dar es Salaam. Msajili wa Hazina, Bw. Nehemiah Mchechu, amekutana na kufanya mazungumzo na wawakilishi wa Barrick Corporation, mwanahisa mwenza wa Twiga Minerals Corporation Limited (TWIGA), pamoja na uongozi wa TWIGA, kujadili maendeleo na masuala mbalimbali yanayohusu uendeshaji wa miradi inayosimamiwa na kampuni hiyo.

Mazungumzo hayo yalifanyika Jumanne, Septemba 1, 2026, wakati ujumbe wa Barrick ulipofanya ziara katika Ofisi ya Msajili wa Hazina (OTR), jijini Dar es Salaam.

Ujumbe wa Barrick uliongozwa na Roelie Gey Von Pittius, Meneja wa Fedha wa Barrick kwa Afrika na Mashariki ya Kati, akiambatana na Candace Simpson, Meneja wa Kodi wa Afrika na Mashariki ya Kati; Melkiory Ngido, Meneja wa Barrick nchini Tanzania; na Judith Chambua, Meneja wa Kodi wa Barrick Tanzania.

Katika kikao hicho, Serikali, kupitia OTR, na Barrick, ambao ni wanahisa wenza wa TWIGA, walijadili masuala mbalimbali yanayohusu maendeleo na uendeshaji wa miradi ya uchimbaji wa dhahabu inayomilikiwa kwa ubia kupitia TWIGA.

Miongoni mwa miradi iliyojadiliwa ni pamoja na migodi ya North Mara na Bulyanhulu, pamoja na Buzwagi, ambao kwa sasa upo katika hatua za mwisho za kufungwa.

Uongozi wa TWIGA pamoja na wataalamu kutoka Barrick walishiriki katika kikao hicho kwa kutoa taarifa na ufafanuzi kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu maendeleo na uendeshaji wa miradi hiyo.

Akizungumza katika kikao hicho, Bw. Mchechu alisema Serikali, kupitia Ofisi ya Msajili wa Hazina, itaendelea kutoa ushirikiano unaohitajika katika kutatua changamoto mbalimbali zinazoweza kujitokeza katika uendeshaji wa miradi ya TWIGA, kwa lengo la kuhakikisha miradi hiyo inaendelea kwa ufanisi, kuongeza uzalishaji na kuchangia zaidi katika uchumi wa Taifa.

Aidha, Bw. Mchechu alisisitiza kuwa sekta ya madini inaendelea kuwa na mchango mkubwa katika uchumi wa Taifa na mapato ya Serikali, ikiwemo kupitia gawio linalotokana na uwekezaji wa Serikali katika kampuni za madini.

Bw. Mchechu alisema Serikali inathamini ushirikiano wake na Barrick na inaendelea kutumia uzoefu uliopatikana kupitia uhusiano huo katika kuimarisha sekta ya madini nchini.

“Tunauthamini sana mchango wa aina ya ushirikiano tulionao na Barrick,” alisema.

Alisema Barrick imekuwa mshirika muhimu katika maendeleo ya sekta ya madini nchini na kwamba ushirikiano huo umeiwezesha Serikali kupata uzoefu katika kusimamia uwekezaji mkubwa katika sekta hiyo.

Bw. Mchechu alisema Serikali inaendelea kufanya mashauriano na taasisi zinazohusika ili kuhakikisha masuala yanayohusu uwekezaji na shughuli za kampuni hiyo yanashughulikiwa kwa ufanisi na kwa uelewa wa pamoja.

“Katika masuala muhimu kama haya yanayomhusu mshirika muhimu katika biashara muhimu, ni lazima serikali izungumze kwa sauti moja,” alisema.

Alisema Serikali inalenga kujenga mazingira yatakayowezesha uwekezaji kuendelea kukua na kutoa manufaa ya muda mrefu kwa Tanzania.

“Tunataka kuwa na biashara ambayo inaweza kuendelea kwa utulivu kizazi hadi kizazi na kustahimili tawala mbalimbali za kisiasa,” alisema.

Kwa upande wake, Von Pittius alisema Barrick inaendelea kuthamini ushirikiano wake na Serikali na inaendelea kushirikiana na mamlaka husika katika masuala yanayohusu shughuli zake nchini.

Bw. Von Pittius alieleza nia ya kuendelea kushirikiana katika masuala mbalimbali yenye maslahi kwa uwekezaji na maendeleo ya sekta ya madini nchini.

Mazungumzo ya Jumanne ni sehemu ya mwendelezo wa ushirikiano kati ya Serikali na Barrick katika kuimarisha mazingira ya uwekezaji na shughuli za madini nchini.








Na Said Mwishehe,Michuzi TV




MAMLAKA ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya(DCEA)imezindua Klabu za kupiga vita dawa za kulevya katika vyuo vikuu nchini ikiwani sehemu ya juhudi za Serikali za kuimarisha ushiriki wa jamii hususani wanafunzi wa vyuo vikuu katika kudhibiti na kupambana na tatizo la dawa za kulevya

Hatua ambayo pia inalenga kuimarisha kinga, kuongeza uelewa na kujenga mazingira yatakayosaidia vijana kufanya maamuzi salama na yenye tija kwa mustakabali wa maisha yao na Taifa kwa ujumla.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa klabu hizo leo Septemba 1,2026 katika ukumbi wa Maktaba Mpya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ,Kamishna Jenerali wa Mamlaka hiyo Aretas Lyimo amesema vilabu hivyo vitatumika pia kutafakari kwa mtizamo wa kitaaluma kuhusu tatizo la dawa za kulevya.

Pia athari zake kwa vijana wa kizazi kipya kwani uraibu ni tatizo linalopoteza utu na kusababisha mateso kwa vijana. “Katika kubabiliana na tatizo hili, kunahitaji majibu ya kina na hatua za uzuiaji zinazohusisha jamii kikamilifu. Vilabu hivi vitatumika pia kwa kutoa elimu na kuhamasisha jamii kuhusu madhara ya dawa za kulevya.

“Tatizo la dawa za kulevya lina athari katika afya ya jamii, usalama, uchumi, familia na maendeleo ya Taifa. Kwa msingi huo, Serikali imeweka mikakati inayolenga kudhibiti biashara na matumizi ya dawa za kulevya.”

Amefafanua mikakati hiyo ni kupunguza upatikanaji wa dawa za kulevya, uhitaji wa dawa za kulevya, madhara yatokanayo na matumizi ya dawa za kulevya pamoja na kuimarisha ushirikiano wa kitaifa, kikanda na kimataifa.

“Tukio lililotukutanisha leo ni sehemu ya utekelezaji wa mkakati wa pili wa kupunguza uhitaji wa dawa za kulevya. Mkakati huu unasisitiza kinga kupitia elimu, uhamasishaji na hatua zinazolenga kuzuia watu kuanza kutumia dawa za kulevya.

“Katika utekelezaji wa mkakati huu, Mamlaka imeandaa muongozo wa utoaji elimu ambao umeainisha makundi yanayohitaji elimu kuhusu tatizo la dawa za kulevya. Wanafunzi wa Vyuo Vikuu ni miongoni mwa makundi hayo muhimu.

“Mamlaka imewalenga wanafunzi wa vyuo vikuu kwa sababu mko katika mazingira ambayo yanahitaji uelewa sahihi na uwezo wa kufanya maamuzi kuhusu masuala yanayoweza kuathiri afya, masomo na mustakabali wenu.

“Tumeshuhudia baadhi ya wanafunzi wa vyuo vikuu wakishindwa kuendelea na masomo yao kutokana na makundi rika na kutumbukia kwenye starehe na matumizi ya dawa za kulevya,”amesema Kamishna Jenerali Lyimo.

Ameongeza pia vyuo vikuu ni vituo vya kuzalisha wataalamu na maarifa yanayosaidia kutatua changamoto mbalimbali za kijamii. Kwa hiyo, elimu kuhusu dawa za kulevya inayotolewa kwa kundi hilo inalenga zaidi kuzuia matumizi ya dawa za kulevya miongoni mwa wanafunzi.

Amesisitiza lengo ni kujenga kizazi cha wataalamu kitakachoweza kulielewa tatizo hili kwa mtazamo wa kitaaluma na kulisaidia Taifa kupata suluhisho lenye ushahidi wa kisayansi ambalo linatumia akili mnemba (AI) na teknolojia katika kupunguza tatizo la dawa za kulevya nchini. Suluhisho la ubunifu wa kimkakati lenye tija kwa Taifa.

“Baada ya kupata elimu hii, Mamlaka inatarajia kuona wanafunzi na wataalamu wa vyuo vikuu wakishiriki katika tafiti kuhusu sababu na vihatarishi vya matumizi ya dawa za kulevya, mwenendo wa tatizo, madhara yake na ufanisi wa hatua zinazochukuliwa katika kukabiliana nalo.

“Tafiti hizo zitasaidia kuongeza uelewa wa Taifa kuhusu tatizo hili na kutoa msingi wa kuboresha sera, mipango na afua za Serikali. Lipo ombwe la tafiti za kisayansi na kitaaluma juu ya tatizo la dawa za kulevya kwa ujumla,”

Amesema hivyo anawahamasisha wanataaluma kujikita kwenye tafiti ili kupata majibu ya kisayansi na kitaaluma juu ya tatizo la dawa za kulevya.”Ninyi kama wataalamu wa afya, mtasaidia katika tafiti kuhusu madhara ya kiafya na tiba…

“Watalaam wa saikolojia na jamii wanaweza kuchunguza sababu zinazochochea matumizi, wataalamu wa sheria wanaweza kusaidia katika kuchambua changamoto za utekelezaji wa sheria huku wataalamu wa TEHAMA wakichangia matumizi ya teknolojia katika kupunguza uingiaji, uzalishaji na usambazaji wa dawa za kulevya”

Awali Mwakilishi wa Jumuiya ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (Vyuo vya kati na Vyuo Vikuu) Tanzania (TAHILISO) Aron Seni amesema vyuo hivyo ni vituo muhimu vya kuzalisha wataalamu na viongozi wa kesho.

Amefafanua lakini mazingira ya sasa yanaweza kuwaweka vijana katika hatari ya kushawishika kutumia dawa za kulevya kutokana na uhuru wa maisha ya chuoni, shinikizo kutoka kwa marafiki na changamoto za maisha.

“Tumeshuhudia baadhi ya vijana kutoka taasisi za elimu ya juu wakikamatwa, kufunguliwa mashtaka na wengine kuhukumiwa kwa makosa yanayohusiana na dawa za kulevya,” amesema.

Ameongeza baadhi ya wanafunzi huanza kutumia dawa hizo kwa majaribio, kushawishiwa na marafiki au kutokana na changamoto mbalimbali za maisha, hivyo hatua za mapema za kinga na elimu zinahitajika.

Amesisitiza klabu hizo hazipaswi kuwa vikundi vya kufanya shughuli za kawaida au kupiga picha kwa ajili ya mitandao ya kijamii, bali ziwe nguzo za elimu, ulinzi na ukombozi wa vijana.

“Klabu hizi zitatoa nafasi salama kwa wanafunzi wanaokabiliwa na changamoto za matumizi ya dawa za kulevya kupata elimu, ushauri na msaada bila kuhukumiwa.Tunaishukuru DCEA kwa ushirikiano uliowezesha kufanikisha mchakato huu.”














Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Nombo,akizungumza wakati akiongoza kikao cha tafakuri cha uongozi na watumishi wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, kilicholenga kutathmini utekelezaji wa majukumu yaliyokabidhiwa kwa wizara.

Na.Mwandishi Wetu

Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Nombo, amewapongeza watumishi wa wizara hiyo kwa kazi kubwa na mafanikio waliyoyapata katika mwaka wa fedha uliopita, huku akiwataka kuendelea kuyasema kwa ujasiri mafanikio hayo yaliyoiwezesha sekta ya elimu kung’aa kitaifa na kimataifa.

Prof. Nombo amesema mafanikio hayo yametokana na uongozi imara wa Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda, na Naibu Waziri, Mhe. Wanu Hafidh Ameir, pamoja na ushirikiano wa Wakurugenzi, Wakuu wa Idara na watumishi wote.

Prof. Nombo amesema hayo Septemba 1, 2026 jijini Dodoma wakati alipoongoza kikao cha tafakuri cha uongozi na watumishi wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, kilicholenga kutathmini utekelezaji wa majukumu yaliyokabidhiwa kwa wizara. Amewashukuru watumishi kwa utekelezaji mzuri wa majukumu yao na kusisitiza umuhimu wa kuendeleza ushirikiano katika kufikia malengo ya wizara.

Aidha, Prof. Nombo amesema mabadiliko makubwa yanayoendelea katika sekta ya elimu yanatokana na utekelezaji wa sera mpya ya elimu, ambayo inalenga kuandaa wahitimu wenye ujuzi, kuboresha matokeo ya kujifunza na kuimarisha mfumo mzima wa elimu nchini. Amesisitiza kuwa Serikali ya Awamu ya Sita, chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, imewekeza kwa kiwango kikubwa katika sekta ya elimu kupitia ujenzi wa miundombinu, ajira za walimu, mafunzo ya watumishi na fursa mbalimbali za kitaaluma.

Katika kikao hicho, Katibu Mkuu amekumbusha wajibu mkubwa wa Wizara katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, akieleza kuwa takribani asilimia 40 ya masuala yaliyomo kwenye dira hiyo yanahusu sekta ya elimu, sayansi, teknolojia na ubunifu. Ameongeza kuwa utekelezaji wa elimu ya lazima kwa miaka 10 na maandalizi ya kupokea kundi la wanafunzi la double cohort mwaka 2028 ni miongoni mwa majukumu makubwa yanayohitaji maandalizi ya mapema na ushirikiano wa pamoja.

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Daniel Mushi, amewataka watumishi kuendelea kufanya kazi kwa ushirikiano, weledi, nidhamu na uadilifu, akisema misingi hiyo ni muhimu katika kuimarisha utendaji kazini. Prof. Mushi amesema hayo Septemba 1, 2026 jijini Dodoma wakati akifunga kikao cha tafakuri cha watumishi wa wizara hiyo.

Amesema mafanikio ya wizara yanatokana na mchango wa kila mtumishi, hivyo kuna umuhimu wa kuongeza ubunifu katika utendaji huku sheria, kanuni, taratibu na miongozo ya utumishi wa umma ikizingatiwa. Pia amesisitiza umuhimu wa kuzingatia usalama wa taarifa za Serikali na kuhakikisha wananchi wanahudumiwa kwa furaha, ufanisi na weledi, huku akiwataka watumishi kutumia mafunzo waliyopata kuongeza tija na kuhamasisha utamaduni wa kuendelea kujifunza katika kila ngazi ya utumishi.

Naye, Mkurugenzi wa Idara ya Utawala na Rasilimali Watu katika Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Edith Rwiza, amesema kikao cha uongozi na watumishi kimetoa fursa ya kutafakari kwa pamoja, kujenga mshikamano na kubadilishana uzoefu kwa lengo la kuimarisha utendaji kazi.

Amesema kikao hicho pia kililenga kutafakari mafanikio, changamoto na mafunzo yaliyopatikana katika utekelezaji wa mipango na majukumu ya wizara katika mwaka uliopita.

Dkt. Rwiza amesema kikao hicho kimewapa watumishi nafasi ya kujitathmini kwa kuzingatia uhalisia wa utendaji kazi na kujadili namna bora ya kuhakikisha malengo ya wizara yanafikiwa kwa ufanisi.

Ameongeza kuwa washiriki wamepata fursa ya kutazama kwa pamoja changamoto za rasilimali na kubaini namna ya kuongeza ufanisi ili kupata matokeov makubwa zaidi kwa kutumia rasilimali zilizopo, huku wakielekezwa kuimarisha mshikamano na uwajibikaji katika kutekeleza majukumu yao.



Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Nombo,akizungumza wakati akiongoza kikao cha tafakuri cha uongozi na watumishi wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, kilicholenga kutathmini utekelezaji wa majukumu yaliyokabidhiwa kwa wizara.



Sehemu ya Watumishi wakimsikiliza Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Nombo (hayupo pichani) wakati akiongoza kikao cha tafakuri cha uongozi na watumishi wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, kilicholenga kutathmini utekelezaji wa majukumu yaliyokabidhiwa kwa wizara.



Sehemu ya Watumishi wakimsikiliza Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Nombo (hayupo pichani) wakati akiongoza kikao cha tafakuri cha uongozi na watumishi wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, kilicholenga kutathmini utekelezaji wa majukumu yaliyokabidhiwa kwa wizara.



Sehemu ya Watumishi wakimsikiliza Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Nombo (hayupo pichani) wakati akiongoza kikao cha tafakuri cha uongozi na watumishi wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, kilicholenga kutathmini utekelezaji wa majukumu yaliyokabidhiwa kwa wizara.



Sehemu ya Watumishi wakimsikiliza Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Nombo (hayupo pichani) wakati akiongoza kikao cha tafakuri cha uongozi na watumishi wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, kilicholenga kutathmini utekelezaji wa majukumu yaliyokabidhiwa kwa wizara.


 Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe. Hamza S. Johari amesema kuwa Serikali inaendelea kufanya maboresho katika Sheria mbalimbali ili kuweka mazingira wezeshi ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050. 

Mwanasheria Mkuu wa Serikali ameyasema hayo tarehe 1 Septemba, 2026 Bungeni Jijini Dodoma,  wakati akiwasilisha Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali wa Mwaka 2026 (The Written Laws (Miscellaneous Amendments) Bill, 2026).

Mhe. Johari ameeleza kuwa ili kuyafikia malengo ya Dira ya Taifa 2050 ni muhimu mfumo wa Sheria uendelee kuhuishwa ili kuendana na mabadiliko ya kiuchumi, kijamii, kiteknolojia na kimataifa, kuondoa vikwazo vya utekelezaji na kuimarisha mifumo ya usimamizi.

"Marekebisho ya sheria ni miongoni mwa hatua muhimu za Serikali katika kuweka mazingira wezeshi ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.” Amesema Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

Akiwasilisha Muswada wa Marekebisho ya Sheria Mbalimbali wa Mwaka 2026 (The Written Laws (Miscellaneous Amendments) Bill, 2026) Mwanasheria Mkuu wa Serikali amezitaja Sheria zilizofanyiwa maboresho ni pamoja na Sheria ya Kuzuia Utakatishaji wa Fedha Haramu, Sura ya 423, Sheria ya Nguvu za Atomiki, Sura ya 188, Sheria ya Benki Kuu ya Tanzania, Sura ya 197, Sheria ya Majina ya Biashara, Sura ya 213, Sheria ya Usafiri wa Anga, Sura ya 80, na Sheria ya Kampuni, Sura ya 212.

Aidha, Mwanasheria Mkuu wa Serikali ameeleza pia Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai, Sura ya 20, Sheria ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya, Sura ya 95, Sheria ya Chuo cha Mipango ya Maendeleo Vijijini, Sura ya 174, Sheria ya Chuo cha Uhasibu Arusha, Sura ya 240, Sheria ya Tafsiri ya Sheria, Sura ya 1, Sheria ya Usimamizi wa Mahakama, Sura ya 237 na Sheria ya Baraza la Vijana, Sura ya 441.

Vilevile, Mhe. Johari amesema kuwa Muswada huo unapendekeza kufanya maboresho pia katika Sheria ya Usajili wa Hataza, Sura ya 217, Sheria ya Magereza, Sura ya 58, Sheria ya Usimamizi wa Maabara Binafsi za Afya, Sura ya 136, Sheria ya Huduma za Maktaba Tanzania, Sura ya 102, Sheria ya Bodi ya Utalii Tanzania, Sura ya 364,





 



NA MWANDISHI WETU

TIMU ya wanawake ya mchezo wa Hockey ya Royal Queens kutoka Zanzibar, imeanza kujiandaa na michuano ya Mapinduzi Cup inayotarajiwa kufanyika mapema mwakani ambapo imefanya mazoezi ya pamoja na wachezaji wa mchezo hao Tanzania Bara.

Akizungumza na gazeti hili jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa Chama cha Hockey Zanzibar , Juma Hassan Juma,amesema ni kwa mara ya kwanza timu ya Hockey ya wanawake kutoka Zanzibar kutua jijini humo kufanya mazoezi ya pamoja na wachezaji wa mchezo huo Tanzania bara.

Amesema , mazoezi hayo ya wiki moja yamekuwa na ufanisi mkubwa katika kuwanoa wachezaji wa timu hiyo ya wanawake.

"Tunaahidi kufanya vizuri katika michuano ya Mapinduzi Cup inayotarajiwa kufanyika Januari mwakani,"amesema Juma.

Ameeleza, changamoto iliyokuwepo awali Zanzibar ni kukosekana kwa viwanja maalumu vya mchezo huo ingawa

kuna mwamko wa jamii kushiriki na kuupenda mchezo huo huku akiishukuru Serikali chini ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi, kuanza ujenzi wa viwanja mbalimbali na hamasa kubwa ya kuinua sekta ya michezo.

Ametoa wito kwa jamii na wahisani kusaidia kukuza mchezo huo wa Hockey hususan timu za majeshi Zanzibar kutoa wachezaji ambao watashiriki katika timu za wanawake za Hockey.

Kipa timu hiyo ya Royal Queens , Idaya Hassan, amesema mazoezi hayo ya pamoja yaliyofanyika katika viwanja vya JMK Youth Park, jijini Dar es Salaam, yamekuwa na ufanisi na yamesaidia wachezaji wa timu yake kujinoa kikamilifu.

Mratibu wa mchezo wa Hockey katika shule za Tanzania Bara , Elieza Mwankemwa, amesema mazoezi hayo ya wiki moja yameambatana na mafunzo mbalimbali kuiimnarisha timu hiyo ya wanawake kwani Zanzibar ilikuwa na timu nyingi za wanaume.








SINGIDA: Mwananchi na mamlaka nchini Tanzania zimetakiwa kuanza kuchukua hatua za mapema kukabiliana na athari zinazoweza kujitokeza kutokana na mvua kubwa na mafuriko yanayoweza kuambatana na hali ya hewa ya El Niño.

Rai hiyo imetolewa na Ndugu Ahmed Misanga wakati akizungumza mkoani Singida, ambapo amesisitiza umuhimu wa maandalizi ya mapema ili kupunguza madhara kwa maisha ya watu, afya, mifugo na mali.

Amesema iwapo mvua kubwa na mafuriko yatatokea, maandalizi ya dharura yanapaswa kuanza kabla ya hali kuwa mbaya, akieleza kuwa hatua hiyo itasaidia kupunguza madhara na kuokoa maisha.

Miongoni mwa hatua alizopendekeza ni kuongeza hifadhi ya chakula na maji salama, pamoja na kuhakikisha hospitali zina dawa na vifaa tiba vya kutosha na kuwa na uwezo wa kuhudumia wagonjwa wengi endapo kutatokea ongezeko la mahitaji ya huduma za afya.

Aidha, Misanga amesisitiza umuhimu wa kuimarisha uwezo wa kudhibiti magonjwa ya mlipuko ambayo yanaweza kujitokeza baada ya mafuriko, huku akipendekeza kuandaliwa kwa kambi za dharura kwa ajili ya wananchi watakaoweza kuathirika.

Amesema pia ni muhimu kuandaa Mobile Health Facilities (Mobile Clinics) zitakazoweza kuwafikia wananchi katika maeneo ambayo huduma za kawaida za afya zinaweza kuvurugwa kutokana na mafuriko.

Katika hatua nyingine, ameitaka jamii na mamlaka kuhakikisha kuna maandalizi ya kutosha ya neti za mbu, mablanketi, mashuka, magodoro na matenti kwa ajili ya waathirika wa mafuriko.

Kwa upande wa uokoaji, Misanga amesisitiza kuimarishwa kwa timu pamoja na vifaa vya uokoaji, huku akitaka maeneo hatarishi yatambuliwe mapema na njia salama za uokoaji ziwekwe wazi.

Amesema mfumo wa tahadhari na utoaji wa taarifa za mapema kwa wananchi nao unapaswa kuimarishwa ili jamii iweze kuchukua hatua kwa wakati pindi kunapokuwa na dalili za hatari.

“Tanzania tusisubiri dharura itokee, tujandae mapema ili tuokoe maisha, afya, mifugo na mali za wananchi,” amesisitiza Misanga.

Akizungumzia mifugo, Misanga amesema maandalizi yanapaswa kuhusisha pia ulinzi wa mifugo dhidi ya mafuriko, magonjwa na upotevu, ikiwa ni pamoja na kuandaa maeneo salama ya kuhamishia mifugo pamoja na kuhakikisha upatikanaji wa chakula, maji na dawa za mifugo.

Amesema mafuriko yanaweza kuleta changamoto mbalimbali kwa jamii, hivyo maandalizi yanapaswa kuwa ya pamoja na kuhusisha sekta za afya, chakula, maji, mifugo na uokoaji.

Amehimiza wananchi na mamlaka kuchukua tahadhari mapema badala ya kusubiri madhara yatokee, akieleza kuwa maandalizi ya wakati yanaweza kuwa hatua muhimu katika kupunguza athari za mafuriko na kulinda maisha pamoja na mali za wananchi.

 

Na Vero Ignatus, Michuzi Tv Arusha

Tanzania imeendelea kuchukua hatua za kuimarisha usalama wa nyuklia na mionzi kuelekea Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2027, ikiwemo matumizi ya vifaa vya kugundua mionzi katika maeneo muhimu na mipakani, pamoja na kuwajengea uwezo maofisa walio mstari wa mbele katika kubaini na kukabiliana na matukio yanayoweza kuhusisha vyanzo vya mionzi.

Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Nguvu za Atomiki Tanzania (TAEC), Profesa Najat Kassim Mohammed, amesema Tanzania kwa kushirikiana na Wakala wa Kimataifa wa Nishati ya Atomiki (IAEA) imeanza kuimarisha maandalizi ya usalama wa nyuklia kuelekea AFCON 2027. Amesema Tanzania ni kiongozi na kinara katika kuhakikisha usalama wa nyuklia na mionzi unazingatiwa katika maandalizi ya mashindano hayo.

Profesa Najat amesema Serikali imewekeza katika wataalamu, vifaa na kujenga uwezo wa kitaifa, huku akisisitiza kuwa ukubwa na hadhi ya AFCON 2027 vinahitaji maandalizi ya kina na ushirikiano wa taasisi mbalimbali. Amesema warsha hiyo inayofanyika Agosti 31 hadi Septemba 4, 2026, imewakutanisha wataalamu na maofisa kutoka JWTZ, Jeshi la Polisi, vyombo vya usalama, mamlaka za forodha na uhamiaji pamoja na wasimamizi wa viwanja vya michezo.

Amesema washiriki wa warsha hiyo watapata mafunzo ya nadharia na vitendo kuhusu utambuzi wa mionzi, tathmini ya tahadhari, upekuzi na matumizi ya vifaa vya kugundua mionzi, ikiwemo Personal Radiation Detectors (PRDs) na Radioisotope Identification Devices (RIDs)

_Mazoezi hayo pia yatahusisha uchunguzi wa kimionzi katika mazingira ya uwanja wa michezo na maeneo ya watazamaji ili kuongeza utayari kuelekea AFCON 2027.

Kwa upande wake, Kiongozi wa Timu ya Wataalamu kutoka IAEA, Lacina Saro, amepongeza Tanzania kwa kuanza mapema maandalizi ya usalama wa nyuklia kuelekea AFCON 2027.

Amesema kuchaguliwa kwa Tanzania kuwa miongoni mwa wenyeji wa mashindano hayo ni jambo la kujivunia, lakini pia kunaambatana na wajibu wa kuhakikisha usalama unaandaliwa mapema, unafanyiwa majaribio na kutekelezwa kwa ufanisi. Ameongeza kuwa IAEA itaendelea kutoa miongozo, mafunzo na msaada wa kiufundi kwa Tanzania.

Naye Mkurugenzi wa Teknolojia na Huduma za Ufundi wa TAEC, Dkt. Remigius Kawala, amesema Tanzania ipo katika nafasi nzuri kutokana na uwekezaji wa Serikali katika wataalamu na vifaa vya usalama wa nyuklia na mionzi. Amesema zaidi ya asilimia 70 ya wataalamu wa TAEC wamebobea katika maeneo yanayohusiana na matumizi ya nguvu za atomu, nyuklia na mionzi, huku Tanzania ikiwa na vifaa vya kutosha vya kutekeleza majukumu ya kiusalama.

Dkt. Kawala amesema Tanzania imeomba msaada wa vifaa kwa kiwango cha chini ya asilimia 20 katika maandalizi ya AFCON 2027, jambo linaloonesha kuwa sehemu kubwa ya mahitaji inaweza kutekelezwa kwa kutumia uwezo na rasilimali zilizopo nchini. Amesema wataalamu wapatao 40 wanashiriki katika maandalizi hayo, huku Tanzania ikiwa ni miongoni mwa nchi wenyeji wa AFCON 2027 pamoja na Kenya na Uganda, ikiwa na lengo la kuhakikisha mashindano yanafanyika katika mazingira salama.

Washiriki wa warsha hiyo watapata mafunzo ya nadharia na vitendo kuhusu utambuzi wa mionzi, tathmini ya tahadhari, upekuzi na matumizi ya vifaa vya kugundua mionzi, ikiwemo Personal Radiation Detectors (PRDs) na Radioisotope Identification Devices (RIDs). Mazoezi hayo pia yatahusisha uchunguzi wa kimionzi katika mazingira ya uwanja wa michezo.










Top News