Naibu Waziri wa Afya na Mbunge wa Jimbo la Muhambwe, Dkt. Florence Samizi, amekabidhi vifaa mbalimbali vyenye thamani ya zaidi ya Shilingi milioni 87 katika maeneo mbalimbali ya Jimbo la Muhambwe, Halmashauri ya Wilaya ya Kibondo, Mkoa wa Kigoma, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa ahadi alizozitoa wakati wa kampeni.

Vifaa vilivyokabidhiwa ni pamoja na mabati 1,050 yenye thamani ya Shilingi milioni 37, saruji mifuko 289 yenye thamani ya Shilingi milioni 6.936, pamoja na kompyuta na printa moja vyenye thamani ya Shilingi milioni 3.5.

Aidha, Dkt. Samizi ametoa zaidi ya Shilingi milioni 40 kwa ajili ya ujenzi wa vivuli katika maeneo ya masoko, hatua inayolenga kuboresha mazingira ya wafanyabiashara na wananchi wanaotumia masoko hayo.

Dkt. Samizi amekabidhi vifaa hivyo akiwa katika ziara ya jimboni kwake, ikiwa ni sehemu ya kuendelea kuwashukuru wananchi kwa ushirikiano wao pamoja na kutekeleza ahadi alizozitoa wakati wa kampeni.

Katika ziara hiyo, Dkt. Samizi amewaasa wananchi kuendelea kutumia fursa zinazopatikana katika kilimo, ikiwemo kulima zao la parachichi, ambalo linaweza kuwa chanzo cha kipato na kuchangia katika kukuza uchumi wa kaya.

Aidha, amewataka wananchi kuchukua tahadhari na kujiandaa kukabiliana na athari zinazoweza kujitokeza kutokana na El Niño, ikiwa ni pamoja na kufuata maelekezo yanayotolewa na mamlaka husika kuhusu hali ya hewa na maandalizi ya kukabiliana na majanga.

Dkt. Samizi amesema Serikali itaendelea kushirikiana na wananchi katika kutatua changamoto zao na kuweka mazingira wezeshi ya maendeleo, huku akisisitiza umuhimu wa wananchi kutumia fursa zinazopatikana katika maeneo yao kwa ajili ya kujiletea maendeleo.






Na Mwandishi Wetu

VIONGOZI nane waliokuwa wakihusika na masuala ya ulinzi na usalama katika ngazi mbalimbali za Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), wamejiunga na Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Miongoni mwa viongozi hao ni aliyekuwa Kaimu Mkuu wa Idara ya Ulinzi na Usalama ya CHADEMA Taifa, Prosper Makonya, ambaye anatajwa kushika nafasi hiyo baada ya kifo cha aliyekuwa Kiongozi wa Idara hiyo, Ali Kibao.

Wanachama hao wamepokelewa na Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa, Itikadi, Uenezi na Mafunzo, Kenani Kihongosi, ambaye aliwaongoza kula kiapo kwa kusoma ahadi za wanachama zilizowekwa katika Katiba ya CCM.

Wengine waliojiunga na CCM ni aliyekuwa Mkuu wa Ulinzi na Usalama Mkoa wa Mwanza, Peter Mashauri; aliyekuwa Mkuu wa Ulinzi na Usalama Jimbo la Kawe, Gibson Mwamaliga; na aliyekuwa Mkuu wa Ulinzi na Usalama Mkoa wa Tanga, Simon Lukindo.

Wengine ni aliyekuwa Mkuu wa Ulinzi na Usalama Jimbo la Korogwe, Sarafu Jengo; aliyekuwa Mkuu wa Ulinzi na Usalama Lushoto, Samwel Sylvester; pamoja na viongozi wengine waliowahi kushika nafasi za ulinzi na usalama katika mikoa ya Simiyu na Morogoro.

Akizungumza wakati wa mapokezi hayo, Makonya, ambaye baada ya kuondoka CHADEMA alijiunga na Chama cha Ukombozi wa Umma (CHAUMMA), alisema ameamua kujiunga na CCM kwa sababu anaamini ni chama chenye uwezo wa kufanya maamuzi na kuyasimamia.

“Ndani ya CCM kuna kila aina ya watu, na ninaweza nikadiriki kusema Chama Cha Mapinduzi ni chama cha Watanzania. Ndani ya CCM kuna maamuzi, wengine wanafuata njia za watu,” alisema.










WAZIRI Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Nchemba, amewasili jijini Roma, Italia, leo Septemba 20, 2026, kumwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika Mkutano wa Kimataifa wa Afya Moja na Mifumo ya Chakula na Kilimo (One Health).

Mkutano huo unatarajiwa kufanyika Septemba 21 hadi 23, 2026, katika Makao Makuu ya Shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo (FAO), jijini Roma.

Akiwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Leonardo da Vinci (Fiumicino), Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu amepokelewa na Waziri wa Kilimo, Mhe. Daniel Chongolo; Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dkt. Ngwaru Maghembe; pamoja na Balozi wa Tanzania nchini Italia, Mhe. Mbarouk Nassor Mbarouk.

Mkutano huo unalenga kujadili masuala ya afya ya binadamu, wanyama na mazingira, pamoja na uhusiano wake na mifumo ya chakula na kilimo duniani.













Na Mwandishi Wetu
WAHITIMU wa Shule ya Msingi na awali ya Pius Pre and Primary school wametakiwa kuendelea kuwa na tabia njema baada ya kupatiwa malezi mazuri Shuleni hapo.

Akizungumza jana katika mahafali yaliyofanyika shuleni hapo Mwalimu Mkuu Sospeter Simon Mabanga amesema Mabanga nendeni mkawe chachu ya maendeleo katika jamii zenu kwani elimu mlizopewa hapa shuleni ni hazina katika familia na taifa kwa ujumla.

Aidha Mabanga ametoa shukrani kwa serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kuruhususekta binafsi kutoa elimu hapa nchini.

Katika mahafali hayo mgeni rasmi alikuwa Dkt. Mwamba Ally Jingu ambaye ni Mhadhiri wa Chuo Kikuu Cha Uhasibu (IFM) ambaye ametoa pongezi kwa uongozi pamoja wa wafanyakazi wote kwa kuwasiamia vema wanafunzi hao

Wakati huohuo zawadi za fedha zimetolewa kwa waalimu ikiwa ni mikakati ya kuinua taaluma na utoaji motisha kwa waalimu kutokana na namna walivyofaulisha kwenye mitihani yao ya taifa.
Shule hiyo ya Pius Pre and Primary iko Kongowe Jijini Dar es Salaam.

Na Mwandishi wetu, Nzega


MWENGE wa uhuru umezindua mradi wa barabara ya lami ya Lumambo - Kitongo yenye urefu wa kilomita 1.750 iliyopo kwenye Kata ya Nzega Mjini Magharibi Mkoani Tabora.

Meneja wa TARURA Wilaya ya Nzega, mhandisi Haruna Mbagalla, akizungumza kwenye uzinduzi wa barabara hiyo amesema lengo la mradi huo ni kurahisisha usafiri na usafirishaji wa bidhaa na abiria katika mji wa Nzega na vitongoji vyake.

Mhandisi Mbagalla amesema ujenzi wake ulianza Mei 12 mwaka 2024 na unatarajiwa kukamilika Desemba 31 mwaka 2026 chini ya mkandarasi Samota Transport Company LTD.

"Gharama za mradi ni shilingi za kitanzania 1,751,051,480.00 fedha kutoka Serikali kuu," amesema mhandisi Mbagalla.

Amesema mradi huo utarahisisha usafiri na usafirishaji wa bidhaa na abiria mji wa Nzega na vitongoji vyake na kuchochea maendeleo, kupunguza gharama za usafiri na usafirishaji na kuboresha mandhari ya mji wa Nzega.

Mkuu wa Wilaya ya Nzega Naitapwaki Lemea Tukai ameishukuru Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kuwapatia fedha za ujenzi na uboreshaji wa barabara za mji wa Nzega.

Kiongozi wa mbio za mwenge wa uhuru kitaifa mwaka 2026 Wazo Michael Mwang'onda amewapongeza TARURA kwa ukamishaji wa barabara hiyo ya lami.

"Pamoja na kuwa barabara hii ipo pembezoni mwa mji wa Nzega ila watu wataitumia na kunufaika nayo ila inavutia na thamani ya fedha inalingana na ubora wake," amesema Mwang'onda.

Kauli mbiu ya mwenge wa uhuru mwaka 2026 ni Tanzania ni yetu sote Tushikamane kwa pamoja kuleta maendeleo''.





Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe Dkt. Samia Suluhu Hassan, akizungumza na Makamu wa Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Uganda, Mhe. Dkt. Speciosa Kazibwe Wandira, wakati wa mazungumzo yao yaliyofanyika Ikulu, Dar es Salaam, Septemba 20, 2026.

Na Munir Shemweta, WANMM

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Dkt. Leonard Akwilapo, amewaagiza Makamishna wa Ardhi Wasaidizi katika mikoa yote nchini kufanya ukaguzi wa maeneo ya uwekezaji yaliyotengwa kwa ajili ya shughuli mbalimbali kwa lengo la kubaini maeneo yasiyoendelezwa na kutoa taarifa ili hatua stahiki zichukuliwe

Dkt. Akwilapo ametoa agizo hilo Septemba 18, 2026, mara baada ya kuhitimisha ziara yake katika maeneo ya uwekezaji ya Kongani ya Viwanda ya KAMAKA pamoja na kiwanda cha Nondo cha Gain Company Limited kilichopo Mlandizi, Wilaya ya Kibaha, Mkoa wa Pwani.

Amesema Wizara ya Ardhi, imebaini kuwepo kwa maeneo ambayo yalipewa wawekezaji kwa ahadi ya kuanzisha viwanda au shughuli nyingine za uzalishaji, lakini hayajaendelezwa kwa muda uliokubaliwa.

“Tuna taarifa kuna waliochukua maeneo wakasema watatengeneza viwanda lakini bado hawajafanya hivyo. Natoa maelekezo makamishna kufanya ukaguzi na kuwasilisha taarifa ili hatua stahiki zichukuliwe kwa maeneo yasiyoendelezwa kadri ya mikataba waliyoingia,” amesema Dkt. Akwilapo.

Aidha, Waziri huyo amewataka wamiliki wote wa ardhi ambao hawazingatii masharti ya uendelezaji maeneo waliyopewa kuhakikisha wanayaendeleza kwa wakati, vinginevyo wizara itachukua hatua kwa mujibu wa sheria na taratibu zilizopo.

Amesisitiza kuwa, hatua hizo zitawahusu wawekezaji wazawa na wa kigeni, akieleza kuwa kwa wawekezaji wazawa hatua inaweza kujumuisha kubadilisha milki za ardhi walizopewa, huku kwa wawekezaji wa kigeni wizara ikishirikiana na taasisi husika, ikiwemo TISEZA, katika kushughulikia masuala ya umiliki na uwekezaji.

Dkt. Akwilapo amesema, hatua hiyo inalenga pia kujibu malalamiko kutoka kwa wananchi ambao maeneo yao yalichukuliwa kwa ajili ya uwekezaji, lakini baadaye hayakuendelezwa.

Ameeleza kuwa, hali hiyo imekuwa ikisababisha wananchi kuhoji sababu za maeneo kutolewa kwa wawekezaji ambao hawajaanza shughuli za maendeleo kwa muda mrefu.

Awali Mhe Dkt Akwilapo alielezwa kuwa eneo la Kongani ya Viwanda Mlandizi wilayani Kibaha mkoa wa Pwani linakabiliwa na changamoto kadhaa kama vile upatikanaji wa maji na ubovu wa barabara hali waliyoieleza kuwa inayosababisha kero katika usafirishaji bidhaa na malighafi.

Hata hivyo, Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) na Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA) wameeleza kuanza  kuchukua hatua za dharura kuhakikisha changamoto hizo zinapatiwa ufumbuzi wa muda mfupi na mrefu

Ziara ya Dkt. Akwilapo katika Mkoa wa Pwani imelenga kujionea kwa karibu shughuli za uwekezaji na matumizi ya ardhi katika maeneo hayo, pamoja na kutathmini namna bora ya kuendeleza maeneo ya uwekezaji kwa kuzingatia mipango ya matumizi ya ardhi na maendeleo endelevu.

Aidha, ziara hiyo ni sehemu ya jitihada za Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi za kutambua fursa na changamoto zinazohusiana na ardhi na uwekezaji, kwa lengo la kuimarisha matumizi bora ya ardhi, kuvutia uwekezaji na kuchochea maendeleo ya wananchi.

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akizungumza wakati wa ziara yake kutembelea Kongani ya Viwanda ya KAMAKA pamoja na kiwanda cha Nondo cha Gain Company Limited Mlandizi, Wilaya ya Kibaha, Mkoa wa Pwani Sept 18, 2026. Kulia ni Mkuu wa Wilaya ya Kibaha Bw. Nickson Simon na kushoto ni Mkurugenzi Mtendaji wa KAMAKA Bw, Yusuf ManziMkuu wa mkoa wa Pwani Mhe, Stanslaus Nyongo akizungumza wakati wa ziara ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo kutembelea Kongani ya Viwanda ya KAMAKA pamoja na kiwanda cha Nondo cha Gain Company Limited Mlandizi, Wilaya ya Kibaha, Mkoa wa Pwani Sept 18, 2026.Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akipata maelezo kuhusiana na kituo kidogo cha kudhibiti umeme kilichopo eneo la Kongani ya viwanda Mlandizi, Wilaya ya Kibaha, Mkoa wa Pwani kutoka kwa Meneja wa Mradi Bw. Leonard Paul Sept 18, 2026.Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akiwa katika kiwanda cha Nondo cha Gain Company Limited wakati wa ziara yake ya kutembelea eneo la Kongani ya viwanda Mlandizi, Wilaya ya Kibaha, Mkoa wa Pwani Sept 18, 2026.Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo (Katikati) akiwa katika picha ya Pamoja na viongozi mbalimbali mkoani Pwani alipotembelea Kongani ya Viwanda ya KAMAKA Mlandizi, Wilaya ya Kibaha, Mkoa wa Pwani Sept 18, 2026. Wa pili kulia ni Mkuu wa Wilaya ya Kibaha Bw. Nickson Simon (PICHA ZOTE NA WIZARA YA ARDHI) 

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema Serikali na taasisi za dini zina wajibu wa kuendelea kushirikiana katika kuimarisha amani, umoja na mshikamano, kukuza maadili mema na kuchangia ustawi wa wananchi.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, tarehe 20 Septemba 2026, katika hafla ya kuwekwa wakfu na kumketisha kitini Mhashamu Askofu Lameck Paul Ndomba kuwa Askofu wa 11 wa Kanisa la Anglikana, Dayosisi ya Zanzibar, iliyofanyika  Kanisa Kuu la Kristo, Mkunazini Wilaya ya Mjini, Mkoa wa Mjini Magharibi.

Amesema Kanisa na taasisi nyingine za dini zina mchango mkubwa katika elimu, afya, malezi, ujenzi wa maadili na maendeleo ya jamii, akisisitiza kuwa tofauti za kiimani zinapaswa kuwa msingi wa kuheshimiana, kuvumiliana na kushirikiana katika kudumisha amani ya Zanzibar.

Rais Dkt. Mwinyi amempongeza Mhashamu Askofu Lameck Paul Ndomba na kumtakia hekima, afya, nguvu na neema ya Mwenyezi Mungu katika kutekeleza majukumu yake ya kuiongoza Dayosisi ya Zanzibar.

Aidha, amesema Serikali itaendelea kushirikiana na Kanisa la Anglikana katika kuhifadhi na kuendeleza maeneo ya kihistoria kwa lengo la kuhifadhi historia ya Zanzibar, kutoa elimu na kukuza utalii wa kihistoria na kiutamaduni.

Akizungumzia hali ya hewa, Rais Dkt. Mwinyi amewahimiza wananchi kuchukua tahadhari na kuzingatia taarifa za Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) kuhusu mvua za Vuli zinazotarajiwa kuathiriwa na hali ya El Niño, huku akizitaka taasisi za dini kushirikiana na Serikali kutoa elimu kwa wananchi kuhusu tahadhari zinazopaswa kuchukuliwa.

Naye , Mhashamu Askofu Lameck Paul Ndomba amemshukuru Rais Dkt. Mwinyi kwa ushirikiano anaouonesha kwa taasisi za dini na juhudi za Serikali katika kuboresha maisha ya wananchi .





















Top News