Na Marco Maduhu, SHINYANGA


WASTAAFU nchini wametakiwa kuwa makini na watu wanaojitambulisha kama mawakala wa Mfuko wa Pensheni kwa Watumishi wa Umma (PSSSF), wakihimizwa kutumia njia rasmi za mfuko huo katika kuhakiki taarifa zao na kufuatilia mafao yao ili kuepuka kutapeliwa na kupoteza fedha zao.


Tahadhari hiyo imetolewa leo, Septemba 18, 2026, na Afisa Msimamizi wa PSSSF Mkoa wa Simiyu, Salum Mwegelo, wakati wa semina ya PSSSF kwa waandishi wa habari kutoka Klabu za Waandishi wa Habari za Shinyanga na Simiyu pamoja na Mtandao wa Wanablogu Tanzania (Tanzania Bloggers Network – TBN), iliyofanyika mjini Shinyanga.


Mwegelo amesema baadhi ya wastaafu wamekuwa katika hatari ya kutapeliwa kutokana na kutumia watu wasio rasmi wanaodai kuwa wanaweza kuwasaidia katika taratibu za kuhakiki taarifa, kufuatilia au kupata mafao yao.


Amesema watu hao wanaweza kuomba taarifa nyeti za wastaafu, ikiwemo namba za siri za akaunti za fedha na taarifa nyingine binafsi, ambazo zinaweza kutumiwa kufanya miamala bila ridhaa ya wahusika.


“Mawakala hao huwarubuni wastaafu na kuomba namba za siri na taarifa muhimu, ikiwemo taarifa za akaunti zao, na kisha kuzitumia kufanya miamala bila ridhaa ya wahusika na kusababisha kupoteza mafao,” amesema Mwegelo.


Mwegelo amesisitiza kuwa PSSSF haina mawakala wanaotoa huduma kwa niaba ya mfuko huo, hivyo wastaafu wanapaswa kuwa na tahadhari dhidi ya mtu yeyote anayejitambulisha kama wakala wa PSSSF na kuwaomba taarifa zao za siri.


Amesema wastaafu wanapaswa kutumia njia rasmi zinazotolewa na PSSSF, ikiwemo kufika katika ofisi za mfuko huo au kutumia mifumo ya kidijitali inayowawezesha wanachama na wastaafu kufuatilia na kuhakiki taarifa zao kwa usalama.


Amesema matumizi ya mifumo ya kidijitali ni miongoni mwa njia zinazoweza kuwasaidia wanachama kupata taarifa zao kwa urahisi bila kulazimika kuwapa watu wengine taarifa zao binafsi au za kifedha.


Kwa upande wake, Afisa Uhusiano wa PSSSF, Abdul Njalo, amewataka waandishi wa habari na wanablogu kutumia taaluma yao kuwafikishia wananchi taarifa sahihi kuhusu huduma za mfuko huo, hususan elimu inayohusu haki, wajibu na taratibu za kupata mafao.

Njalo amesema vyombo vya habari, blogu na majukwaa ya kidijitali vina nafasi kubwa katika kuhakikisha elimu hiyo inawafikia wanachama na wastaafu kwa lugha rahisi na inayoeleweka, huku akiwataka waandishi na wanablogu kuthibitisha taarifa kabla ya kuzifikisha kwa umma.


Amesema elimu sahihi inaweza kusaidia kuwawezesha wanachama na wastaafu kutambua njia halali za kupata huduma za PSSSF na kuchukua tahadhari dhidi ya watu wanaoweza kutumia mwanya wa ukosefu wa taarifa kuwahadaa.


Naye Mwenyekiti wa Klabu ya Waandishi wa Habari Mkoa wa Shinyanga, Greyson Kakuru, amesema semina hiyo imekuwa na umuhimu mkubwa kwa waandishi wa habari na wanablogu kwa kuwa imewapa uelewa zaidi kuhusu huduma za PSSSF na masuala yanayowahusu wanachama na wastaafu.


Kakuru amesema maarifa yaliyopatikana yatawasaidia waandishi na wanablogu kuandaa na kusambaza habari zenye usahihi, huku wakitoa elimu kwa jamii kuhusu namna ya kutumia huduma za PSSSF na kujilinda dhidi ya utapeli.


Amesema ushirikiano kati ya PSSSF na vyombo vya habari pamoja na wanablogu ni muhimu katika kuhakikisha wananchi wanapata taarifa sahihi kwa wakati na kutumia huduma za hifadhi ya jamii kwa uelewa zaidi.


Naye Mratibu wa Tanzania Bloggers Network (TBN) Kanda ya Ziwa, Kadama Malunde, amepongeza PSSSF kwa kuandaa semina hiyo, akisema mafunzo kama hayo ni muhimu kwa waandishi wa habari na wanablogu kwa kuwa yanawaongezea uelewa wa masuala wanayopaswa kuyafikisha kwa jamii.


Malunde amesema waandishi na wanablogu wana wajibu mkubwa wa kuhakikisha kila taarifa wanayoitoa kwa umma inathibitishwa, ina usahihi na inatoka katika vyanzo vinavyoaminika, hususan katika kipindi hiki ambacho taarifa za kidijitali zinaweza kusambaa kwa kasi kubwa.


“Semina kama hii ni muhimu kwa sababu inatupa nafasi ya kujifunza na kuongeza uelewa. Tukiwa waandishi na wanablogu, jukumu letu si kuchapisha taarifa tu, bali kuhakikisha taarifa tunazowafikishia wananchi ni sahihi, zimehakikiwa na zina manufaa kwa jamii,” amesema Malunde.







Na Mwandishi Wetu

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Dkt. Leonard Akwilapo, amewaonya wananchi wanaovamia maeneo kwa nguvu na kuunda vikosi vya ulinzi kwa ajili ya kulinda maeneo hayo, akisema Serikali haitavumilia vitendo hivyo na kwamba hatua kali za kisheria zitachukuliwa.

Dkt. Akwilapo ametoa onyo hilo leo Sept 17, 2026 wakati akizungumza na wananchi katika Kliniki ya Ardhi iliyofanyika Kata ya Zingiziwa, Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam.

Amesema, wananchi hawapaswi kujichukulia sheria mkononi kwa kuvamia maeneo yanayomilikiwa na watu wengine na kuanzisha vikosi vya ulinzi kwa lengo la kuyadhibiti kwa nguvu.

“Serikali haitavumilia vitendo vya watu kujichukulia sheria kwa kuvamia maeneo ya wananchi wengine na kuunda vikosi vya ulinzi kwa lengo la kulinda maeneo hayo kwa nguvu,” amesema Dkt. Akwilapo.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam, Bw. Elihuruma Mabelya, amesema hadi sasa jumla ya hati miliki 545 zimetolewa kwa wananchi kupitia Kliniki hiyo ya Ardhi.

Mabelya ameeleza kuwa, timu ya wataalamu itaendelea kuwepo katika eneo hilo ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma za ardhi kwa urahisi na kwa wakati, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa maelekezo ya Wizara.

Baadhi ya wananchi, kupitia Diwani wa Kata hiyo, wameipongeza Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa kusogeza huduma za ardhi karibu na maeneo yao.

Wameielezea hatua hiyo kuwa imewapunguzia adha ya kusafiri umbali mrefu pamoja na gharama kubwa walizokuwa wakitumia ili kufuata huduma hizo.Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Dkt. Leonard Akwilapo, akizungumza na wananchi waliojitokeza katika Kliniki ya Ardhi iliyofanyika Kata ya Zingiziwa, Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam, leo Septemba 17, 2026.




Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Dkt. Leonard Akwilapo, akikabidhi hati kwa baadhi ya wananchi waliokamilisha taratibu za umiliki wa ardhi na waliojitokeza katika Kliniki ya Ardhi iliyofanyika Kata ya Zingiziwa, Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam, leo Septemba 17, 2026.

Sehemu ya wananchi waliojitokeza katika Kliniki ya Ardhi iliyofanyika Kata ya Zingiziwa, Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam, leo Septemba 17, 2026.

Na. Jawadu Kinyobwa

 Serikali imesema itaendelea kushirikiana na Chama Cha Wafanyakazi Madaktari na Wafamasia Tanzania katika kushughulikia changamoto zinazowakabili wataalamu hao, huku ikisisitiza umuhimu wa maslahi ya watumishi kwenda sambamba na utoaji wa huduma bora kwa wananchi.

Hayo yamebainishwa na Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Ndege Qwaray, wakati akifungua Mkutano Mkuu wa Pili wa Chama cha Wafanyakazi wa Madaktari na Wafamasia Tanzania, leo Septemba 18, 2026. 

Amesema Serikali inatambua nafasi ya vyama vya wafanyakazi katika kujenga mahusiano bora kazini, kuwakilisha maslahi ya wanachama na kusaidia kutafuta suluhisho la changamoto zinazojitokeza katika maeneo ya kazi.

Amesema Serikali imeendelea kuongeza uwekezaji katika Sekta ya Afya, ambapo idadi ya vituo vya kutolea huduma imeongezeka kutoka 10,153 mwaka 2021/22 hadi 13,683 Machi 2026, sawa na ongezeko la vituo 3,530.

 Aidha, Serikali imejenga hospitali mpya 10 za rufaa za mikoa, kukarabati hospitali kongwe 50, kukamilisha maboma 980 ya zahanati na kujenga vituo vipya vya afya 390, sambamba na kuongeza vifaa tiba vya kisasa ikiwemo CT Scan na MRI.

Katika eneo la rasilimali watu, Mhe. Qwaray amesema Serikali imeajiri zaidi ya watumishi wa afya 53,633 wa kada mbalimbali katika kipindi cha mwaka 2021 hadi 2025/26. 

Mhe. Qwaray amesisitiza kuwa Serikali inatambua mchango wa Madaktari na Wafamasia katika kujenga Taifa lenye afya bora na itaendelea kushirikiana na chama hicho pamoja na wadau wengine wa Sekta ya Afya katika kutafuta ufumbuzi wa changamoto zilizopo. 

Amesema katika kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, ni muhimu waendelee kujenga utaalamu, kufanya tafiti, kubuni njia mpya za utoaji huduma na kutumia teknolojia kuboresha afya za wananchi.








 



Rais Mstaafu Dkt Jakaya Mrisho Kikwete akipokea tuzo kutoka kwa Mwenyekiti wa Kairuki Health and Education Network Bi Kokushubira Kairuki katika maadhimisho ya Mwezi wa Uelewa wa Saratani ya Tezi Dume yaliyofanyika katika Hospitali ya Kairuki, Mikocheni, jijini Dar es salaam jana.


RAIS Mstaafu wa Awamu ya Nne, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, amewataka wanaume kujenga utamaduni wa kupima afya ya tezi dume mara kwa mara, akisema uchunguzi wa mapema huongeza uwezekano wa kupata matibabu kwa wakati kabla saratani haijasambaa.

Dkt. Kikwete ametoa wito huo jijini Dar es Salaam alipokuwa mgeni rasmi katika maadhimisho ya Mwezi wa Uelewa wa Saratani ya Tezi Dume yaliyofanyika katika Hospitali ya Kairuki, Mikocheni.

Katika maadhimisho hayo, Dkt. Kikwete alitembelea mtambo wa kisasa wa High Intensity Focused Ultrasound (HIFU), unaotumika kutibu baadhi ya uvimbe, ikiwamo saratani ya tezi dume kwa wagonjwa wanaostahili, bila kufanyiwa upasuaji wa kawaida. Teknolojia hiyo hutumia mawimbi ya sauti yenye nguvu kuelekeza joto katika eneo lenye uvimbe.

Akizungumza kuhusu uzoefu wake binafsi, Dkt. Kikwete alisema alipogundulika mapema kuwa na dalili za saratani ya tezi dume mwaka 2014, aliamua kufanyiwa uchunguzi wa kina nchini Marekani. Vipimo vilichukuliwa na kuthibitisha kuwa saratani ilikuwa katika hatua za awali, hali iliyomwezesha kuchukua hatua za matibabu mapema.

“Walichukua sampuli 14 na katika sampuli mbili wakaona dalili za saratani. Madaktari wakaniambia kuwa ilikuwa inaanza na kwamba ingeweza kutibika,” alisema.

Alisema alikubali kufanyiwa upasuaji wa kuondoa tezi dume ili kuzuia saratani hiyo isisambae katika sehemu nyingine za mwili, na kwamba tangu wakati huo ameendelea kuwa na afya njema.

“Baada ya kufanyiwa upasuaji nilijenga utaratibu wa kupima afya yangu mara kwa mara. Kwa sasa afya yangu ni njema kabisa; ndiyo maana mtu akisema ninaumwa, nacheka tu, kwa sababu ninaifahamu afya yangu,” alisema.

Mkuu wa mkoa wa Tanga, Balozi Dkt. Batilda Burian akizungumza katika semina ya PSSSF kwa maafisa Rasilimaliwatu wa mkoa wa Tanga kilichofanyika mapema leo Septemba 17, 2026 ikiwa na lengo la kuwaelimisha huduma mbalimbali zitolewazo na Mfuko na hasa kuwahamasisha kuwasilisha madai ya wanachama kwa wakati na matumizi ya kidigitali.
Afisa Mfawidhi wa Mkoa wa Tanga, Bi. Hanim Babika akizungumza katika semina ya PSSSF kwa maafisa Rasilimaliwatu na Utawala wa mkoa wa Tanga..
Meneja wa PSSSF Kanda ya Kaskazini Mashariki, Bw. Kwame Temu akizungumza katika semina kwa maafisa Rasilimaliwatu na Utawala wa Mkoa wa Tanga.
Picha ya pamoja Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Balozi Dkt. Batilda Burian Meneja wa PSSSF Kanda ya Kaskazini Mashariki, Bw. Kwame Temu wakiwa na maofisa wa PSSSF na washiriki wa semina ya PSSSF kwa maafisa Rasilimaliwatu na Utawala wa mkoa wa Tanga.


Na Mwandishi wetu, Tanga
MKUU wa Mkoa wa Tanga, Balozi Dkt. Batilda Burian amewataka wastaafu kulinda mafao yao dhidi ya matapeli, huku akiupongeza Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) kwa kuhamasisha matumizi ya mifumo ya kidijitali inayorudisha heshima na tabasamu kwa wastaafu.

Akifungua semina ya PSSSF kwa waajiri iliyofanyika jijini Tanga iliyowakutanisha Maafisa Rasilimaliwatu na Utawala 120 kutoka taasisi mbalimbali za Serikali, Balozi Dkt. Batilda alieleza kuwa maboresho hayo yanaendana na maagizo ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kutoa huduma bora, za haraka na bila vikwazo. "Niwapongeze sana PSSSF kwa hatua hii inaowezesha Mafao kulipwa kwa haraka," alisema.

Meneja wa PSSSF Kanda ya Kaskazini Mashariki, Bw. Kwame Temu, aliwahimiza waajiri kutoa taarifa za watumishi wapya ndani ya siku 30 ili wasajiliwe mapema na kuwahamasisha watumishi kutumia kikamilifu mifumo ya kielektroniki. Kwa upande wake, Afisa Mfawidhi wa Mkoa wa Tanga, Bi. Hanim Babika, alisisitiza waajiri kufanyia kazi changamoto ya kugongana kwa taarifa na kuhakikisha wafanyakazi wa mikataba kusajiliwa.

Akitoa ushuhuda, Katibu Tawala wa Mkoa wa Tanga, Bw. Rashid Mchatta alisema elimu inayotolewa na PSSSF imebadili kabisa maisha ya wastaafu wa sasa, kwani wanatoka utumishi wakiwa wanajiamini na wenye uelewa mpana wa uwekezaji. "Sekretari wangu alipostaafu, alikuja ofisini kwangu mwenye furaha, ananieleza habari za fursa za uwekezaji tu baada ya kupata mafunzo ya PSSSF," alisema Katibu Tawala.

PSSSF inaendelea kuwasihi wanachama na wastaafu nchini kutumia mifumo rasmi ya kielektroniki ili kupata huduma kwa haraka, uwazi na usalama zaidi ambayo ni PSSSF Member Portal na PSSSF Kiganjani, aidha wawawe na changamoto kutumia simu ya bure kuwasiliana na Mfuko ambazo ni 0800110055.

Na Mwandishi wetu.
KATIKA habari njema kwa Tanzania na sekta ya fedha barani Afrika, Nicomed Bohay ameteuliwa kuwa Mkurugenzi Mtendaji Mkuu wa EFAfrica Group Ltd (Group CEO), kampuni ya Pan-Afrika inayojihusisha na ufadhili wa mashine na vifaa vya uzalishaji kwa wakulima, viwanda, biashara, ujenzi na usafirishaji.

Uteuzi huo unamfanya Bohay kuwa Mtanzania anayeongoza taasisi yenye shughuli zake nchini Tanzania, Kenya, Zambia na Mauritius, huku akipewa jukumu la kuongoza mkakati wa kupanua huduma za leasing na kuongeza upatikanaji wa mashine za uzalishaji kwa maelfu ya wafanyabiashara na wakulima barani Afrika.

Akizungumza kuhusu uteuzi huo, Mwenyekiti Mtendaji wa EFAfrica Group, Dk. Michiel Timmerman, alisema Bohay ameonyesha uwezo mkubwa wa uongozi, nidhamu katika usimamizi wa taasisi na dhamira ya kuleta matokeo yanayogusa maisha ya wananchi.

 “Nicomed ameonyesha uongozi wa kipekee, nidhamu katika usimamizi na dhamira ya kweli ya kuimarisha ujumuishi wa kifedha kupitia ufadhili wa vifaa vya uzalishaji. Tuna imani kuwa ataiongoza EFAfrica kufikia hatua mpya ya ukuaji na athari kubwa zaidi kwa wakulima na biashara za Afrika,” alisema Dk. Timmerman.

Bohay ni mtaalamu wa fedha za maendeleo mwenye uzoefu wa karibu miaka 30 katika sekta ya benki, biashara za kilimo na maendeleo ya ujasiriamali. Kabla ya kujiunga na EFAfrica mwaka 2021, aliwahi kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa PASS Trust Tanzania, ambako aliongoza programu mbalimbali za kuwawezesha wajasiriamali wa kilimo na kusaidia kuanzishwa kwa Agribusiness Innovation Centre.

Pia aliwahi kuongoza Idara ya Biashara za Kilimo katika Benki ya CRDB, akichangia kwa kiasi kikubwa kuimarisha upatikanaji wa mitaji kwa wakulima na biashara zinazohusiana na kilimo nchini Tanzania.

Mwaka 2021, Bohay aliteuliwa kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Equity for Tanzania Limited (EFTA). Ndani ya kipindi chake cha uongozi, kampuni ilipanua huduma zake kwa kiwango kikubwa na kujiimarisha kama taasisi inayoongoza nchini katika ufadhili wa mashine za uzalishaji kupitia mfumo wa leasing.

Mbali na ukuaji wa biashara, EFTA iliendelea kuwa na ubora wa hali ya juu wa mikopo, ambapo taarifa za fedha za Juni 2026 zilionyesha kiwango cha mikopo chechefu cha asilimia 1 pekee.

Moja ya mafanikio makubwa ya Bohay ni kusimamia ufadhili wa zaidi ya mashine 4,000 za kilimo nchini Tanzania. Mashine hizo zinajumuisha matrekta, power tillers, combine harvesters, mifumo ya umwagiliaji na vifaa vingine vilivyosaidia kuongeza uzalishaji, kupunguza gharama za kilimo na kuimarisha usalama wa chakula.

Lakini mafanikio hayo hayakuishia mashambani. Kupitia mfumo wa leasing, EFTA imewezesha maelfu ya biashara kupata malori, mabasi, mashine za viwandani, vifaa vya ujenzi na mitambo ya uchakataji, hatua iliyochochea ukuaji wa biashara na kuongeza ajira katika sekta mbalimbali za uchumi.

Katika kuendeleza ujumuishi wa kiuchumi, Bohay pia alisimamia kuanzishwa kwa Mpango wa Ukodishaji wa Vifaranga na Chakula cha Kuku, uliolenga wanawake na vijana.

Kupitia programu hiyo, wanufaika hupata vifaranga vya siku moja, chakula na pembejeo muhimu kwa mfumo wa leasing bila kuhitaji mtaji mkubwa wa kuanzisha biashara, hivyo kuwapa fursa ya kujiajiri na kuongeza kipato.

Akizungumza baada ya uteuzi wake, Bohay alisema lengo lake ni kuhakikisha upatikanaji wa mashine za uzalishaji hauwi tena kikwazo kwa maendeleo ya Waafrika.

 “Tunataka EFAfrica iwe mshirika wa kwanza wa wakulima na wafanyabiashara katika safari yao ya ukuaji. Tukiwapa watu vifaa vya kuzalisha, tunawapa uwezo wa kubadilisha maisha yao, kuunda ajira na kuchochea uchumi wa Afrika,” alisema Bohay.

Uteuzi wa Nicomed Bohay unaendelea kuipa Tanzania heshima katika sekta ya fedha na maendeleo, huku ukitoa ujumbe kwamba wataalamu wa Kitanzania wanaweza kuongoza taasisi kubwa za Pan-Afrika na kuchangia moja kwa moja katika mageuzi ya uchumi wa bara.

Na Victor Masangu, Kibaha

Mstahiki Meya wa Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha Dkt. Nicas Mawazo amewahimiza wazazi na walezi kuachana na tabia ya kuwatelekeza watoto wao hasa katika suala zima la kuwaendeleza kielimu  na badala yake  washiriki   kikamilifu katika kuwa mstari wa mbele kuchangia maendeleo   katika  kuboresha   sekta ya elimu na sio kubaki nyuma.

Kauli hiyo imetolewa na mstahiki Meya wa Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha wakati wa mahafali  ya 16  shule ya msingi Lulanzi Dkt. Nicas Mawazo ambapo amewahimiza wazazi wanapaswa kuweka misingi imara ya kuchangia elimu kwa ajili ya kuweza kuwasaidia watoto wao wasome katika mazingira mazuri na  kutimiza ndoto zao ambazo wamejiwekea.

"Kwanza  nimefarijika sana kualikwa katika mahafali haya ya darasa la saba katika shule ya msingi Lulanzi lakini kitu kikubwa ambacho ninawaomba  wazazi na walezi ni lazima tushirikiane kwa pamoja katika suala zima la kuweza kuchangia mambo mbali ya kielimu na lengo kubwa ni kwa ajili ya watoto wetu ikiwa sambamba na kuboressha miundombinu ya shule pamoja na ujenzi wa ofisi za walimu,"amebainisha Mstahiki Meya.

Mstahiki Meya huyo amebainisha kwamba lengo lake kubwa ni kuendelea kushirikiana bega kwa bega na wazazi pamoja na walezi  kwa lengo la kuleta mabadiliko chanya ya kuboresha elimu katika shule mbali mbali zilizopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha na kuahidi kuendelea kutoa sapoti lengo ikiwa ni kuweka mipango madhubuti ya kukuza elimu na wanafunzi kusoma katika mazingira mazuri.

Kwa upande wake Mkuu wa shule ya msingi Lulanzi Bakari amesema kwamba shule hiyo inakabiliwa na changamoto mbali mbali ikiwemo sula la kukosa uzio pamoja na mahitaji mengine  ya msingi  hivyo ameimba serikali kuweza kuwasaidia kwa hali na mali ili walimu na wanafunzi waweze kusoma katika mazingira ambayo ni rafiki.

Naye mmoja wa wanafunzi ambao wamehitimu katika shule hiyo Janeth Mwangi akisoma risala kwa niaba ya wanafunzi wenzake amebainisha kwamba shule hiyo tangu ianzishwe mnamo mwaka 2007 imeweza kupata mafanikio makubwa ikiwemo katika kufanya vizuri katika nyanja ya kitaaluma pamoja na  uboreshaji wa mazingira ya shule.

"Tangu shule hii ilipoanzishwa mnamo mwaka 2007 imeweza kupiga hatua kubwa sana ikiwemo suala la uboreshaji wa miundombinu ya shule japo tunakabiliwa na uhaba wa fedha kwa ajili ya uendeshaji wa shule, uwepo wa wingi wa wanafunzi upungufu mbali mbali wa vifaa vya taaluma,"amebainisha Mwalimu huyo.

Mahafali ya 16 ya shule hiyo  ya msingi ya Lulanzi   iliyopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha imeweza kuhudhuliwa  na wageni mnbali mbali wakiwemo  viongozi mbali mbali wa serikali, viongozi wa chama pamoja na wazazi na walezi kwa lengo la kuweza kushiriki  na kujumuika katika mahafali hayo ya  darasa la saba.

                                                            



Kampuni ya Sandaland Fashion Wear Limited  imetangaza kuchukua hatua za kisheria dhidi ya kauli iliyotolewa hadharani na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda, kuhusu jezi za Timu ya Taifa ya Tanzania, Taifa Stars.

Hatua hiyo imetangazwa kupitia tamko rasmi la kampuni hiyo, baada ya kauli ya Makonda iliyotolewa Septemba 16, 2026 kupitia akaunti yake ya Instagram, ambapo alidai kuwa imeathiri jina, chapa, hadhi na uhalali wa bidhaa za Sandaland katika soko.

Katika ujumbe huo, Makonda alinukuliwa akisema:

“Hii sio jezi ya Taifa Stars, Taifa Stars kwa ubora wake hatuwezi kuwa na jezi za kiwango chini hivi. Acheni kutumia picha za Naibu wangu huku ofisi yangu haina taarifa.”

Ujumbe huo uliambatana na picha ya Naibu Waziri Hamis Mwinjuma, maarufu Mwana FA, akiwa amevalia jezi yenye mchanganyiko wa rangi ya njano, bluu, nyeusi na kijani.

Kwa upande wake, Sandaland imesema kauli hiyo imezua taharuki na sintofahamu, huku ikidai kuwa tayari imesababisha madhara ya kiuchumi na kuathiri hadhi ya kampuni.

Kampuni hiyo imeeleza kuwa ina mkataba halali na Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) wa kutengeneza na kusambaza jezi za Taifa Stars, ambazo zimetumika katika mashindano mbalimbali ya timu za taifa za wanaume na wanawake.

Sandaland imeongeza kuwa haitanyamaza na inakusudia kuchukua hatua za kisheria dhidi ya kauli hiyo, ikidai kuwa ilitolewa kwa namna inayoweza kuchafua chapa yake.

Aidha, kampuni hiyo imesisitiza kuwa imejenga jina na heshima yake kwa muda mrefu na imepewa dhamana ya kushughulikia jezi za Taifa Stars.



Na Farida Said Morogoro

Mkuu wa Wilaya ya Kilosa, Mhe. Shaka Hamdu Shaka, leo ameongoza kikao cha Kamati ya Ushauri ya Kodi ya Wilaya kilichofanyika katika Ofisi ya Mkuu wa Wilaya.

Kikao hicho kimejadili tathmini ya mwenendo wa makusanyo ya mapato kwa mwaka wa fedha 2025/2026 na kuweka mikakati ya kuimarisha makusanyo kwa mwaka 2026/2027.Akizungumza katika kikao hicho, Shaka amesema kazi ya kukusanya kodi sio ukusanyaji tu, bali ni ujenzi wa maendeleo.

"Sisi sio wakusanya kodi tu, bali ni wajenzi wa maendeleo. Kila shilingi tunayokusanya kwa haki na uadilifu, tunajenga kesho bora ya wananchi wetu. Hivyo jukumu letu sio dogo," alisema Shaka.

Aidha, Shaka ameelekeza kila chanzo cha mapato Wilayani humo kipitiwe upya.

"Kile ambacho kimekufa kifufue, kile ambacho kinalala kiamshwe. Lazima tubadili mtazamo kutoka kudhibiti kwenda kuelimisha umma," alisisitiza.

Ameitaka TRA na Halmashauri kuimarisha matumizi ya takwimu halisi (Data) na kufunga mihuri yote ya uvujaji wa mapato.

"Mapato yanayokusanywa lazima yaingie yote. Tunahitaji uwazi wa mifumo ya ukusanyaji wa kielektroniki. Wilaya ya Kilosa ina uwezo wa kukusanya zaidi ya mara mbili ya tunayokusanya sasa, kama watendaji wataamua kuwa wabunifu na waadilifu," alifafanua.

Shaka amemalizia kwa kusema, "Tusiogope kufanya mapitio magumu. Bora kuwa na vyanzo 20 hai vinavyoingiza kuliko kuwa na vyanzo 100 hewa vinavyotupa sifa bandia."

Naye Katibu wa kikao hicho, Meneja wa TRA Kilosa, Bi. Saada Mtoto, amesema TRA katika kipindi kilichopita imevuka malengo ya ukusanyaji na kuahidi kufanyia kazi maelekezo yote yaliyotolewa ili kufikia malengo endelevu.






MKURUGENZI wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai, Kamishna wa Polisi Ramadhani Kingai, amegoma kutoa ushahidi kwa upande wa utetezi wa Mwenyekiti wa Chadema, Tundu Lissu, anayekabiliwa na mashtaka ya uhaini katika Mahakama Kuu Masijala Ndogo Dar es Salaam.

Hatua hiyo imempelekea mshtakiwa Lissu, ambaye anajitetea mwenyewe katika kesi hiyo, kufunga ushahidi wa upande wa utetezi.

Kesi hiyo leo, Septemba 18, 2026, iliitwa mahakamani hapo kwa ajili ya kuendelea na ushahidi wa upande wa utetezi, ambapo DCI Kingai alitarajiwa kutoa ushahidi.

Akizungumza mbele ya Jopo la Majaji linaloongozwa na Jaji Dustun Ndunguru, Lissu amedai amekutana na DCI Kingai, ambaye alikuwa amependekeza awe shahidi wake wa leo, ndani ya chumba cha mahakama na kuzungumza naye kwa kina kuhusu suala la kutoa ushahidi kwa upande wa utetezi.

Amedai kuwa baada ya kumweleza Kingai maeneo ambayo angependa ayatolee ushahidi, shahidi huyo alimweleza kuwa hawezi na hayuko tayari kutoa ushahidi kwa upande wa utetezi.

“Mimi nimemuelewa kama hayuko tayari, siwezi kumlazimisha kutoa ushahidi ambao hayupo tayari kuutoa,” amedai Lissu.

Amedai Kingai amemweleza kuwa yeye yuko upande wa watu wanaoomba na watakaoshangilia endapo atapatikana na hatia, hivyo hayuko tayari kutoa ushahidi kwa niaba yake.

“Yeye yuko upande wa wale wanaoomba na watakaoshangilia nikipatikana na hatia, kwa hiyo amesema hayuko tayari kuja kutoa ushahidi kwa niaba yangu,” amedai Lissu.

Amedai Kingai pia amemweleza kuhusu mashahidi wengine wawili ambao ni Mkuu wa Majeshi, CDF Jacob Nkunda, na Mkuu wa Jeshi la Polisi, IGP Camilius Wambura, ambao pia mahakama iliamuru wapelekewe wito, kuwa nao watakaporejea nchini na kupata wito wa mahakama, msimamo wao utakuwa kama wake.

“Kwamba na wao hawatakuwa tayari kutoa ushahidi kwa upande wa utetezi, hawawezi kwa sababu ile ile ya wale wanaoombea na watakaoshangilia nikipatikana na hatia,” amedai Lissu.

Kutokana na hali hiyo, Lissu amesema hana mashahidi wengine wa kuwaita na hivyo ameomba kufunga ushahidi wa upande wa utetezi.

Baada ya kusikiliza maelezo hayo, kesi hiyo sasa imefungwa kwa pande zote mbili na kuomba kupangiwa siku ya kuwasilisha hoja za mwisho.

Upande wa utetezi umeeleza kuwa ratiba ya kikao cha mahakama inaishia Septemba 25, hivyo kubaki siku saba za kuandaa hoja za mwisho.

Lissu amesema yuko tayari kuwasilisha hoja hizo Jumatano, huku akieleza kuwa mwenendo wa kesi una hoja zaidi ya kurasa 1,000.

Upande wa Jamhuri umekubaliana na Lissu kuhusu tarehe hiyo na kueleza kuwa utakuwa tayari kwa ajili ya kuwasilisha hoja za mwisho.

Kesi imeahirishwa hadi Septemba 23, 2026. 



Na Janeth Raphael – MichuziTv

Wakala wa Vipimo (WMA) umewataka wafanyabiashara na wananchi kuacha kutumia madebe, makopo, mafungu na vifaa vingine visivyotambuliwa kisheria kama vipimo katika biashara, ukieleza kuwa matumizi ya vifaa hivyo ni kinyume cha sheria na yanaweza kuchukuliwa kuwa kosa la jinai.

Akizungumza leo jijini Dodoma katika mkutano na waandishi wa habari kuhusu utekelezaji wa majukumu ya Wakala kwa mwaka wa fedha 2025/26 na mwelekeo wa mwaka 2026/27, Afisa Mtendaji Mkuu wa WMA, Alban Kihulla, amesema vipimo visivyo rasmi vinaweza kusababisha bidhaa kupimwa kwa viwango tofauti na hivyo kuwanyima haki watumiaji.

Kihulla amesema matumizi ya madebe na makopo katika kupima bidhaa kwa uzito hayatoi kipimo cha uhakika kwa kuwa kiasi kinachopatikana kinaweza kutofautiana kutoka chombo kimoja hadi kingine, jambo linaloweza kusababisha mfanyabiashara au mlaji kupata kiwango kisicho sahihi cha bidhaa anayolipia.

“Madebe, makopo, visado na mafungu sio vipimo na tumeendelea kutoa elimu kwa wananchi, lakini pia tunaendelea kuchukua hatua dhidi ya wanaojihusisha na upimaji wa aina hiyo,” amesema Kihulla.

Amesema WMA itaendelea kusimamia matumizi ya vipimo sahihi kwa lengo la kuhakikisha biashara zinafanyika kwa haki na kulinda maslahi ya wafanyabiashara pamoja na watumiaji, huku akiwataka wafanyabiashara kuhakikisha wanakuwa na mizani inayokidhi matakwa ya kisheria katika maeneo yao ya biashara.

Aidha, Kihulla amewahimiza wananchi kujenga utamaduni wa kuhakikisha bidhaa wanazonunua zinapimwa kwa mizani sahihi, akisisitiza kuwa matumizi ya vipimo vinavyotambulika kisheria ni sehemu muhimu ya kulinda haki za mlaji na kuhakikisha kila mmoja anapata kiwango cha bidhaa anachostahili.



Na Janeth Raphael - MichuziTv

Wakala wa Vipimo (WMA) umesema jukumu la kuhakikisha vipimo vinavyotumika katika biashara vinafanyika kwa usahihi, pamoja na kutekelezwa kwa mujibu wa sheria, lina msingi pia katika mafundisho yanayopatikana katika vitabu vya dini, ikiwemo Qur’an Tukufu na Biblia Takatifu.

Afisa Mtendaji Mkuu wa WMA, Alban Kihulla, ameyasema hayo leo jijini Dodoma wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu utekelezaji wa majukumu ya Wakala kwa mwaka 2025/26 pamoja na mwelekeo wa utekelezaji kwa mwaka 2026/27.

Kihulla amesema maandiko matakatifu yanasisitiza umuhimu wa kufanya vipimo kwa usahihi, hivyo wafanyabiashara wanapaswa kuhakikisha wanatumia vipimo sahihi na vilivyohakikiwa kwa mujibu wa sheria. Amesema hatua hiyo ni muhimu katika kujenga uadilifu na kuaminiana katika shughuli za biashara.

“Mtu anayetaka kufanya biashara afanye biashara iliyonyooka. Lazima awe na vipimo sahihi na ambavyo vimehakikiwa kwa mujibu wa sheria,” amesema Kihulla.

Amesema WMA, ikiwa ni sehemu ya safari ya kuelekea utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050, itaendelea kuhakikisha vipimo vinavyotumika katika shughuli mbalimbali vinaendana na viwango vinavyotakiwa. “Kilo moja ukipimiwa kweli iwe kilo moja, na si vinginevyo,” amesema.

Kwa mujibu wa Kihulla, usimamizi wa vipimo unalenga kujenga uaminifu katika biashara, kumlinda mlaji pamoja na mtoa huduma, huku ukiisaidia Serikali kupata mapato yanayostahili kupitia matumizi ya vipimo sahihi na vilivyohakikiwa.

Amesema WMA itaendelea kuwa chombo muhimu katika kuwezesha utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050, hususan katika kujenga mazingira ya biashara yenye uaminifu na hatimaye kuchangia ujenzi wa Taifa lenye uchumi imara, jumuishi na wenye ushindani.




NA MWANDISHI WETU, DODOMA

Wananchi na viongozi wa Zanzibar wamepongezwa kwa kufikia muafaka wa kitaifa kwa kuimarisha umoja na mshikamano kuelekea ujenzi wa taifa lenye maendeleo.

Hayo yameelezwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake wa Chama Cha Mapinduzi (UWT) Taifa na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu (MCC), Mary Chatanda, Septemba 18, 2026, Jijini Dodoma.

Chatanda amesema, hakuna shaka kuwa, wananchi na viongozi wa Zanzibar, wamesukumwa na dhamira ya dhati ya ujenzi wa taifa lao badala ya kutanguliza tofauti zao za kisiasa na maslahi binafsi.

"Niwapongeze wananchi na viongozi wa Zanzibar ambao waliangalia maendeleo badala ya tofauti zao za vyama, waliangalia Zanzibar waitakayo yenye neema na ustawi badala ya misuguano isiyokwisha, ndiyo maana wakaona wakae pamoja, waelewane ili kuunganisha nguvu ya pamoja katika kusukuma mbele gurudumu la maendeleo," amesema Chatanda.

Aidha, Chatanda amempongeza Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Dkt. Hussein Mwinyi kwa kuwa na hekima, busara na utulivu huku akiwashirikisha kikamilifu viongozi wastaafu na wengine kutoka vyama vya upinzani katika kutafuta muafaka wa pamoja ili Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK) iundwe na kufanya kazi.

"Rais Dkt. Hussein Mwinyi ameonyesha ukomavu mkubwa wa kiuongozi, kwa kweli nampongeza sana. Vilevile, niwapongeze wanasiasa hasa kutoka Chama cha ACT- Wazalendo, kwa kukubali kukaa meza moja ya mazungumzo ili muafaka upatikane, hatimaye Zanzibar isonge mbele kimaendeleo. Kwa kweli Wazanzibar wamethibitisha kuwa inawezekana kufikia muafaka wa kitaifa kupitia meza ya mazungumzo," amesema.

Ikumbukwe kuwa, tangu kumalizika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba, 2025, kumekuwa na mazungumzo ya pamoja yanayoendelea ili kukamilisha uundwaji wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa baina ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na ACT - Wazalendo.

Septemba 17, 2026, Kamati ya Uongozi ya ACT- Wazalendo, ilikaa kikao maalum kilichofanyika ofisi ndogo za Chama hicho, Vuga Mjini Unguja, ambapo pamoja na mambo mengine, kilifanya uteuzi wa jina la mwanachama anayependekezwa kuwa Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar.

Kufuatia kikao hicho, Septemba 18, 2026, Rais Dkt. Hussein Mwinyi, alifanya uteuzi wa Othman Masoud Othman, kuwa Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, ambapo ataapishwa rasmi Septemba 22, 2026, Ikulu, Zanzibar.

Kukamilika kwa mchakato wa upatikanaji wa Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, kunaendeleza mchakato wa kuteua mawaziri kutoka ACT- Wazalendo ili kukamilisha uundwaji wa serikali ya pamoja ambayo itakuwa chachu ya kuendeleza mipango mizuri ya maendeleo kwa manufaa ya wananchi wa Zanzibar huku umoja, amani, upendo na mshikamano ukiwa nguzo kuu ya maendeleo hayo.


Na Victor Masangu, Kibaha

Mbunge wa viti maalumu Mkoa wa Pwani kupitia chama cha mapoinduzi (CCM) Mariamu Ulega katika kuunga mkono juhudi za seriklai katika kuboresha sekta ya elimu ameahidi kuchangia kiasi cha shilingi milioni 2 kwa ajili ya kuboresha miundombinu katika shule ya msingi ya Mkoani B iliyopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha hususan katika suala la ujenzi wa kujenga uzio.

Akizungumza wakati wa mahafali ya kwanza kwa mchepua wa kiingereza katika shule ya msingi Mkoani B Katibu wa Jumuiya ya umoja wa wanawake (UWT) Mkoa wa Pwani Aziza Hussein kwa niaba ya mgeni rasmi Mbunge wa viti maalumu Mariamu Ulega ambaye pia Mke wa Waziri wa Ujenzi Abdalah Ulega.

Katibu huyo huyo wa UWT Mkoa akitoa salamu za Mbunge huyo amebainisha kwamba anatambua umuhimu mkubwa wa suala zima la elimu hivyo ameamua kuchangia kiasi hicho cha shilingi milioni 2 ambazo zitaweza kusaidia katika mwendelezo wa ujenzi wa uzio katika shule hiyo ya msingi Mkoani B yenye mchepuo wa kiingereza.

"Nashukuru sana nimeweza kushiriki na kualikwa katika mahafali haya ya kwanza katika shule hii ya msingi mkoani B lakini mimi ni Katibu wa UWT Mkoa wa Pwani lakini kwa leo nimepewa heshima ya kipekee kwa ajili ya kuweza kumwakilisha Mbunge wa viti maalumu mheshimiwa Mariamu Ulega ambaye yeye ndiye aliyetakiwa kuwa mgeni rasmi katika sherehe hizi z amahafali,"amebainisha Katibu huyo.

Aidha katibu huyo ameongeza kwamba lengo kubwa ni kuendelea kushirikiana bega kwa bega na walimu, wazazi pamoja na wadau mbali mbali wa maendeleo katika kutoa sapoti na michango yao ambayo itaweza kusaidia katika kukuza sekta ya elimu sambamba na kuboresha zaidi miundombinu katika shule hiyo.

"Mbunge wenu wa viti maalumu mheshimiwa Mariam Ulega ameniagiza kuja kumwakilisha na amesema yupo pamoja nanyi na kwamba amesema kuwa anachangia kiasi cha shilingi milioni mbili na na kuelekeza kwamba fedha hizo zitumike katika kuboresha miundombinu ya ujenzi wa uzio ili watoto hao waweze kusoma katika mazingira ambayo ni rafiki na salama na kwamba ataendelea kuisaidia shule hiyo katika mambo mengine mbali mbali,"ameongeza Katibu huyo.

Katika hatua nyingine amempongeza kwa dhati Rais wa awamu ya sita Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuweza kutenga fedha nyingi ambazo zimeweza kuleta mabadiliko makubwa katika kutekelza miradi ya maendeleo hususan kuboresha sekta ya elimu ikiwemo ujenzi i wa madarasa pamoja na madawati.

Pia katibu huyo mbali na kutoa salamu za mheshimiwa Mbunge wa viti maalumu Mariamu Ulega amesema na wao kama uongozi wa UWT Mkoa wa Pwani wameamua kuchangia kiasi cha shilingi laki tano ikiwa ni moja na jitihada za kuunga mkono juhudi ambazo zinafanywa na Rais Dkt Samia Suluhu Hassan katika kuboresha sekta ya elimu hapa nchini.

Nao baadhi ya wazazi na walezi akiwemo Teodory Joseph pamoja na Joseph Ogutu wameipongeza serikali kwa kuweza kuboresha sekta ya elimu huku wakiiomba kuweka misingi madhubuti ya kuendelea kutenga shule nyingine na kuziingiza katika progamu hiyo ya kuwa na mchepuo wa masomo ya kiingereza.

Mahafali ya kwanza ya kwa mchepuo wa kiingereza katika shule ya Msingi Mkoani B iliyopo Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha Mkoa wa Pwani imeweza kuhudhuliwa na viongozi mbali mbali wa serikali, wazazi na walezi pamoja na wadau wengine mbali mbali wa maendeleo katika sekta ya elimu.



Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Paul Christian Makonda, ametangaza kutoutambua mchakato wa kubadilisha jezi za timu za taifa, akisema umefanyika bila kuishirikisha Wizara licha ya maelekezo aliyoyatoa Februari 2026.

Sambamba na hatua hiyo, Waziri Makonda ameagiza kuundwa kwa kamati maalumu itakayochunguza mikataba ya wazabuni wa jezi hizo, manufaa yake kwa timu za taifa pamoja na mapato yatokanayo na mauzo ya jezi.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Wizara hiyo leo, Septemba 18, 2026, uchunguzi huo unalenga kubaini iwapo mikataba iliyopo inanufaisha timu za taifa kwa kiwango kinacholingana na fedha nyingi zinazotolewa na Serikali kugharamia timu hizo.

Taarifa hiyo imeeleza kuwa Februari 2026, Waziri Makonda alitoa maelekezo ya kuboresha jezi za timu za taifa ili ziakisi utambulisho wa Tanzania na kuzalisha manufaa mapana zaidi kwa nchi.

Hatua hiyo inatajwa kuwa muhimu kutokana na uwekezaji mkubwa unaofanywa na Serikali katika maandalizi ya timu za taifa zinazoshiriki mashindano ya kimataifa, pamoja na maandalizi ya Tanzania kuwa mwenyeji mwenza wa mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika mwaka 2027 (AFCON 2027).

Wizara imebainisha kuwa jezi za timu za taifa hazipaswi kuangaliwa kama mavazi ya wachezaji pekee, bali pia kama sehemu ya utambulisho wa taifa na chanzo cha mapato yanayoweza kusaidia uendeshaji wa timu hizo.

“Pamoja na kutoutambua utambulisho wa jezi za timu ya taifa, Waziri Makonda ataunda Kamati ya kuchunguza mikataba ya mzabuni wa jezi hizo, ili kubaini manufaa ya mikataba hiyo kwa timu za taifa ambazo zimekuwa zikigharimiwa na Serikali kwa fedha nyingi,” imeeleza sehemu ya taarifa hiyo iliyosainiwa na Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini Bi Zaituni Mkwama. 

Kamati hiyo pia itachunguza namna mapato yanayotokana na mauzo ya jezi za timu za taifa yanavyokusanywa na mchango wake katika kugharamia shughuli za timu hizo.


Top News