Na Victor Masangu, Kibaha

Jumuiya ya umoja wa wanawake (UWT) Wilaya ya Kibaha mjini kwa kushirikiana na wadau wengine wa maendeleo wakiwemo Azania bank wameamua kuungana kwa pamoja na kuitoa darasa la mafunzo kwa wajasiriamali kutoka kata zote 14 kwa lengo la kuweza kuwapa ujuzi wa kutengeneza bidhaa mbali mbali ambazo zitawasaidia kujikwamua kiuchumi.

Akizungumza katika ziara maalumu ya kikazi yenye lengo la kuweza kutoa mafunzo hayo Mwenyekiti wa UWT Wilaya ya Kibaha mjini Elina Mgonja amebainisha kwamba ameamua kutoa darasa hilo ikiwa ni ahadi yake ambayo aliitoa wakati wa zira ya kushukuru wanawake kwa kuweza kuipigia CCM kura za kishindo katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2025.

Mwenyekiti Mgonja amesema kwamba ametembelea wanawake hao na kutoa fursa za mafunzo ya ujarisiamali kwa kuwafundisha jinsi ya kutengeneza bidhaa za aina tofauti zikiwemo utengenezaji wa sabubi kwa ajili ya kufulia nguo , sabuni ya kuogea, na namna ya kutengeneza batiki pamoja na utengenezaji wa bidhaa nyingine.

"Nikiwa kama Mwenyekiti wa UWT Wilaya ya Kibaha mjini nimeamua kutimiza ahadi yangu ya kuwapa mafunzo ya ujariamali bure wanawake kutoka kata zote 14 zilizopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha na mafunzo haya pia nimeshirikiana na wenzetu wa Azania bank ambao na wao wameweza kutoa elimu ya jinsi ya kutunza fedha na kujikwamua kiuchumi,"amebainisha Mwenyekiti Mgonja.

Kwa upande wake Afisa Mahusiano wa Azania Bank Happiness Lema amebainisha kwamba lengo lao kubwa la kushirikiana bega kwa bega na Jumuiya ya ya wanawake wa UWT Wilaya ya Kibaha mjini kwa lengo la kuwasaidia kuwapa elimu ya kujikwamua kichumi ikiwemo pamoja na suala zima la utunzaji wa fedha.

"Sisi kama Azania bank tumeoana kuna umuhimu mkubwa wa kuweza kushirikiana na Jumujiya ya wanawake wa UWT Wila ya Kibaha mjini na tumeamua kutembea nao katika ziara yakeo yenye lengo la kutoa darasa maaalumu kwa ajili ya kuwafundisha jinsi ya kutengeneza bidhaa na sisi kama benki tumewafundisha namna bora ya kujikomboa kiuchumi pamoja na jinsi ya kutumia fursa za mikopo yenye liba nafuu,"amenainisha Happiness.

Ziara ya Mwenyekiti wa UWT Wilaya ya Kibaha mjini ya kutoa mafunzo kwa wanawake wajasiriamali kwa sasa inaendelea kufanyika ambapo hadi sasa imeshapita katika kata tisa ambazo ni Msangani, Mkuza, Maili moja, Tumbi, Viziwaziwa, Kibaha, Kongowe, Misugususgu pamoja na Kata ya Visiga.






Kizimkazi, Unguja 📍

Wakala wa Nishati Vijijini (REA) umefanikiwa kusambaza takribani mitungi laki saba ya gesi ya kupikia (LPG) nchini kote, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa kasi wa Mkakati wa Kitaifa wa Nishati Safi ya Kupikia.

Hayo yameelezwa na Mkurugenzi wa Nishati Jadidifu na Teknolojia za Nishati Jadidifu kutoka REA, Mhandisi, Advera Mwijage, wakati akizungumza kwenye mdaharo maalum uliofanyika katika Tamasha la Kizimkazi mkoani wa Kusini Unguja, Zanzibar; Mhandisi Advera alimwakilisha Mkurugenzi Mkuu wa REA, Mhandisi Hassan Saidy.

Mhandisi Advera alieleza kuwa mafanikio hayo yametokana na uwezeshaji mkubwa kutoka kwa Serikali ya Awamu ya Sita, pamoja na uwepo wa vyanzo vingi vya nishati nchini. Alibainisha kuwa REA ilitumia majukwaa ya Waheshimiwa Wabunge kusambaza mitungi hiyo ili kuwafikia wananchi wa ngazi ya chini na kutoa elimu ya matumizi ya nishati hiyo.

"Miradi hii ikiwemo ya gesi ya kupikia (LPG) na majiko banifu inatolewa kwa njia ya ruzuku. Bila ruzuku kwa wananchi wa vijijini, mabadiliko ya kuelekea nishati safi yatachukua muda mrefu sana," alisema Mhandisi Advera.

Kuhusu utunzaji wa mazingira, Mhandisi Advera alisema REA imeanzisha mradi wa kusambaza majiko banifu ili kupunguza kasi ya uharibifu wa misitu. Inakadiriwa kuwa takribani hekta 470,000 za misitu hukatwa kila mwaka nchini kwa ajili ya kuni na mkaa.

Ili kukabiliana na changamoto hiyo, REA imeshirikiana na Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) kufungua viwanda vya kuzalisha mkaa mbadala maeneo ya vijijini, tofauti na hapo awali ambapo viwanda hivyo vilikuwa vimejificha mijini. Hatua hiyo imefanya mkaa mbadala kupatikana kwa gharama nafuu vijijini.

Katika hatua nyingine, REA kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), imefanikiwa kuunganisha jumla ya wateja 1,001 wa majumbani na taasisi kwenye mkuza wa mabomba ya Gesi Asilia katika mikoa ya Lindi na Pwani.

Mhandisi Advera alitoa wito kwa wananchi ambao bado hawajafikiwa na miradi hiyo kuendelea kuwa wavumilivu, kwani utekelezaji unaenda kwa awamu kulingana na ukomo wa bajeti ya serikali. Lengo kuu la serikali ni kuhakikisha zaidi ya asilimia 80 ya Watanzania wanatumia nishati safi ya kupikia.

Mdaharo huo ulihudhuriwa na viongozi waandamizi wa sekta ya nishati, akiwemo Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, Naibu Waziri Mhe. Salome Makamba, na Katibu Mkuu (Umeme na Nishati Jadidifu) Mhandisi Felchesmi Mramba.

Viongozi wengine waliohudhuria na kushiriki ni pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Bw. Lazaro Twange, huku mdaharo huo ukianzishwa na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati Mstaafu, Mhe. Doto Biteko, Mbuge wa Jimbo la Bukombe.









 

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema Tamasha la Kizimkazi limeendelea kuwa jukwaa muhimu la kutangaza utamaduni, utalii, biashara na fursa za uwekezaji zilizopo Zanzibar, sambamba na kuchochea maendeleo ya wananchi.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, tarehe 12 Agosti 2026, alipokuwa akizindua rasmi Tamasha la Kizimkazi 2026 lenye kaulimbiu “KIZIMKAZI Kumenoga!” katika Mkoa wa Kusini Unguja.

Amepongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa maono ya kuasisi Tamasha hilo, ambalo limekuwa likichangia kuhifadhi mila na utamaduni, kukuza utalii na kufungua fursa za kiuchumi kwa wananchi.

Aidha, Rais Dkt. Mwinyi amesisitiza umuhimu wa kutumia Tamasha hilo kutangaza fursa za uwekezaji katika utalii, uvuvi, mwani na Uchumi wa Buluu, huku Serikali ikiendelea kuimarisha mazingira ya uwekezaji na miundombinu ya uzalishaji.

Amesema Tamasha la Kizimkazi linaunga mkono dhamira ya Serikali ya kuongeza idadi ya watalii wanaotembelea Zanzibar kutoka 800,000 hadi milioni 1.5, kupitia matukio maalum ya utalii na utangazaji wa vivutio, utamaduni, vyakula na ukarimu wa Wazanzibari.

Rais Dkt. Mwinyi amewapongeza waandaaji, wadhamini, taasisi za Serikali, Sekta Binafsi, wajasiriamali, wasanii, wanamichezo na wananchi kwa kufanikisha Tamasha la Kizimkazi 2026, akihimiza kuendelea kulitumia kama jukwaa la kufungua fursa mpya za maendeleo.

Tamasha hilo linaendelea hadi tarehe 14 Agosti 2026, ambapo kilele chake kitafanyika katika Uwanja wa Mwehe, Kizimkazi, Mkoa wa Kusini Unguja.



















Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) imesisitiza dhamira yake ya kuendelea kuunga mkono juhudi za Serikali na wadau mbalimbali katika kukuza matumizi ya nishati safi ya kupikia, kuhifadhi mazingira, kukuza utalii na kuendeleza ubunifu wa vijana, ikieleza kuwa maeneo hayo ni sehemu muhimu ya kujenga uchumi endelevu na wenye fursa kwa vizazi vya sasa na vijavyo.

Dhamira hiyo imebainishwa jana na Mkurugenzi Mtendaji wa NBC, Bw. Theobald Sabi, wakati wa hafla maalum ya mnada wa sanaa za picha iliyoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, iliyofanyika katika Hoteli ya Kwanza, Kizimkazi, Zanzibar.

Hafla hiyo, iliyoandaliwa na Mwanamke Initiative Foundation (MIF) kwa kushirikiana na kampuni ya ubunifu ya Waba Group, ilihusisha mnada wa picha zilizopigwa katika maeneo mbalimbali ya Zanzibar, zikionesha mandhari, utamaduni, maisha ya jamii, utalii na urithi wa asili wa visiwa hivyo.

Akizungumza katika hafla hiyo, Rais Samia aliwataka wadau wanaojihusisha na sanaa ya upigaji picha, hususan vijana, kutumia ubunifu wao zaidi katika kutangaza utalii wa Tanzania, akibainisha kuwa sekta hiyo ina fursa kubwa za kibiashara na inaweza kuwa chanzo muhimu cha ajira na kipato.

“Zaidi nawapongeza sana vijana walioshiriki katika upigaji wa picha hizi kwa ubunifu na uwezo wao wa kutumia picha kusimulia uzuri, utamaduni na maisha ya Tanzania. Kazi zao hizi zinaweza kuwa sehemu muhimu ya kutangaza nchi na pia kuwa chanzo cha mapato,” alisema Rais Samia.

Rais Samia pia alieleza kuvutiwa na ubunifu wa wapiga picha walioshiriki, akitaja miongoni mwa kazi zilizomvutia picha za pomboo (Dolphin) chini ya bahari, wanawake wenye asili ya Pwani wakilima mwani pamoja na mandhari mbalimbali za Zanzibar.

“Picha hizi zimenifurahisha sana kwa sababu zinatangaza mandhari za Zanzibar, utalii, utamaduni, mila na desturi zetu,” alisema.

Aidha, Rais Samia aliwashukuru wadau walioshiriki katika kufanikisha hafla hiyo, ikiwemo benki ya NBC ambayo ilikuwa miongoni mwa wadhamini muhimu wa tukio hilo.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Mwanamke Initiative Foundation, Bi. Wanu Hafidh Ameir (Mb), alisema fedha zitakazopatikana kupitia mnada huo zitaelekezwa katika kuunga mkono jitihada za kukuza matumizi ya nishati safi ya kupikia, kupunguza utegemezi wa nishati zinazochangia ukataji wa misitu na hivyo kusaidia uhifadhi wa mazingira na bioanuwai.

“Sanaa na mazingira ni vitu viwili vinavyokwenda sambamba. Tunaweza kutumia sanaa katika kuhamasisha na kukusanya fedha kwa ajili ya kutunza mazingira. Fedha zitakazopatikana katika mnada huu zitasaidia harakati za upatikanaji wa nishati safi ya kupikia, kulinda mazingira na kutangaza utalii,” alisema Bi. Wanu.

Akizungumzia nafasi ya NBC katika kuunga mkono agenda ya nishati safi ya kupikia, Sabi alisema benki hiyo iko tayari kushirikiana na wadau mbalimbali katika kuwezesha mnyororo mzima wa nishati hiyo, kuanzia uzalishaji hadi matumizi.

“Sisi NBC, mtazamo wetu ni kufadhili mnyororo mzima wa nishati safi ya kupikia. Kwetu sisi huu ni zaidi ya ushiriki—ni sehemu ya dhamira yetu ya kujenga jamii endelevu, kulinda mazingira na kuunga mkono ubunifu unaobeba suluhisho kwa kizazi cha sasa na kijacho,” alisema Sabi.

Sabi aliongeza kuwa NBC inaona fursa kubwa katika sekta ya sanaa za picha, akisema picha zina uwezo mkubwa wa kujenga na kusambaza simulizi kuhusu utamaduni, sanaa na utalii wa Tanzania.

Alisema uwekezaji katika sekta hiyo unaweza kuwa sehemu ya fursa za biashara za kisasa zenye uwezo wa kukua ndani na nje ya nchi, huku ukichangia kuitangaza Tanzania kama moja ya vivutio muhimu vya utalii duniani.

“Picha ina uwezo wa kusema mengi bila kutumia maneno mengi. Tunapoibua vipaji vya vijana na kuwawezesha kutumia sanaa ya picha, tunakuwa pia tumewekeza katika kuitangaza Tanzania, utamaduni wetu na fursa zetu za utalii kwa hadhira ya ndani na kimataifa,”

“Kwa NBC, ushiriki huo unaendelea kuakisi dhamira ya benki ya kutumia nguvu ya biashara, ubunifu na ushirikiano wa wadau kuchangia maendeleo endelevu, uhifadhi wa mazingira na ujenzi wa fursa mpya kwa vijana.” alisema Sabi.

Mbali na kushiriki katika hafla hiyo, NBC ilikuwa miongoni mwa wadhamini muhimu wa tukio hilo na ilitunukiwa tuzo maalum ya kutoka kwa Rais Samia ikiwa ni utambuzi wa mchango wake katika kufanikisha hafla hiyo na kuunga mkono ajenda ya maendeleo endelevu, ikiwemo jitihada za kukuza nishati safi ya kupikia na uhifadhi wa mazingira.

Hafla hiyo pia ilitoa jukwaa kwa vijana kuonesha vipaji vyao katika sanaa ya upigaji picha. Zaidi ya vijana 200 walihusika katika mchakato wa kushiriki katika mpango huo, huku kazi za wapiga picha 15 zikichaguliwa na jumla ya picha 10 zikifanikiwa kuuzwa kupitia mnada huo.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan (kulia) akimkabidhi Mkurugenzi Mtendaji wa NBC, Bw. Theobald Sabi tuzo maalum ya kutambua mchango wa benki hiyo katika kufanikisha maandalizi ya hafla maalum ya mnada wa sanaa za picha uliolenga kukusanya fedha kwa ajili ya kuunga mkono jitihada za kukuza matumizi ya nishati safi ya kupikia, kupunguza utegemezi wa nishati zinazochangia ukataji wa misitu na hivyo kusaidia uhifadhi wa mazingira na bioanuwai kupitia taasisi ya Mwanamke Initiative Foundation (MIF). Hafla hiyo ilifanyika katika Hoteli ya Kwanza, Kizimkazi, Zanzibar jana.


Akizungumzia nafasi ya NBC katika kuunga mkono agenda ya nishati safi ya kupikia, Mkurugenzi Mtendaji wa NBC, Bw. Theobald Sabi (alieshika mic) alisema benki hiyo iko tayari kushirikiana na wadau mbalimbali katika kuwezesha mnyororo mzima wa nishati hiyo, kuanzia uzalishaji hadi matumizi.






Akiwa kwenye hafla hiyo Mkurugenzi Mtendaji wa NBC, Bw. Theobald Sabi alipata wasaa wa kubadilisha mawazo na viongozi pamoja na wadau mbalimbali.

Mkurugenzi wa Wateja Wakubwa na Uwekezaji, Bw. Elvis Ndunguru (katikati) alipata wasaa wa kubadilisha mawazo na viongozi pamoja na wadau mbalimbali.

Mkuu wa Idara ya Mawasiliano na Mahusiano ya Umma wa Benki ya NBC, Bw Godwin Semunyu (kushoto) akifuatilia hafla hiyo.



📌 Asema wajibu wa kila Mtanzania ni kuhakikisha mafanikio yanakuwa endelevu

KIZIMKAZI, ZANZIBAR

Naibu Waziri Mkuu Mstaafu na Mbunge wa Jimbo la Bukombe, Mhe. Dkt. Doto Biteko, amesema Tanzania imepiga hatua kubwa katika utekelezaji wa Ajenda ya Nishati Safi ya Kupikia, huku akisisitiza kuwa ni wajibu wa kila Mtanzania kuhakikisha mafanikio yaliyopatikana yanaendelea kuwa endelevu.

Dkt. Biteko amesema hayo wakati akishiriki mjadala kuhusu “Uongozi wa Kimkakati wa Tanzania katika Kuharakisha Mabadiliko ya Nishati Endelevu na Jumuishi”, uliofanyika katika Mdahalo wa Nishati Safi ulioandaliwa na Taasisi ya Mwanamke Initiative Foundation (MIF), Kizimkazi, Mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar.

Amesema uwepo wa Mkakati wa Taifa wa Nishati Safi ya Kupikia ni sehemu ya jitihada za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye ameendelea kuipa msukumo ajenda hiyo katika ngazi mbalimbali za uongozi wake na kuifikisha hadi katika majukwaa ya kimataifa.

Dkt. Biteko amesema umuhimu wa kuendelea kuipa kipaumbele ajenda hiyo unatokana na ukubwa wa athari za matumizi ya nishati isiyo safi ya kupikia, ikiwemo uharibifu wa mazingira unaosababishwa na matumizi ya kuni na mkaa, ambapo takribani hekta 470,000 za misitu hupotea kila mwaka nchini.

Aidha, amesema zaidi ya watu 33,000 hupoteza maisha kila mwaka kutokana na magonjwa yanayohusishwa na uchafuzi wa hewa wakati wa kupika, hali inayoonesha umuhimu wa kuongeza kasi ya mpito kuelekea matumizi ya nishati safi.

Ameongeza kuwa matumizi ya nishati isiyo safi yana athari za kijinsia, hususan kwa wanawake ambao hutumia muda mwingi kutafuta kuni badala ya kushiriki kikamilifu katika shughuli za uzalishaji na maendeleo ya kiuchumi.

Amesema athari hizo pia zinawagusa watoto, ambapo baadhi yao hukosa muda wa kutosha wa kuhudhuria masomo kutokana na kulazimika kusaidia familia zao kutafuta kuni kwa ajili ya kupikia.

Katika mjadala huo, Dkt. Biteko amesisitiza umuhimu wa kufanya tathmini za mara kwa mara ili kubaini kiwango cha uendelevu wa matumizi ya nishati safi ya kupikia, hususan baada ya wananchi kuwezeshwa kupata teknolojia na miundombinu husika.

Amesema tathmini hizo zitasaidia Serikali na wadau kubaini changamoto zilizopo, kupima matokeo yaliyofikiwa na kuweka mikakati madhubuti zaidi ya kuendeleza matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini.

Pia, Dkt. Biteko ameipongeza Taasisi ya Mwanamke Initiative Foundation (MIF) kwa kuwa miongoni mwa taasisi zinazochangia utekelezaji wa Ajenda ya Nishati Safi ya Kupikia kupitia shughuli mbalimbali, ikiwemo kusaidia upatikanaji wa miundombinu pamoja na kuendesha midahalo inayowakutanisha wadau kujadili namna bora ya kuharakisha matumizi ya nishati safi, salama na endelevu nchini.


NA: MWANDISHI WETU

Kodi ni chanzo muhimu cha mapato kinachoiwezesha serikali kufanikisha mipango na mikakati yake ya kimaendeleo kwa wananchi wake.

Wananchi wanahitaji huduma nzuri za kijamii kama elimu, afya, maji, umeme, barabara na masoko. Aidha, wanahitaji pia kuwezeshwa kiuchumi kwa kupatiwa mikopo nafuu ya kuwawezesha kujikwamua kiuchumi kwa kuanzisha shughuli za kibiashara na za kiujasiriamali.

Ni kwamba, mambo haya mazuri na mengine mengi, hayawezi kufanikiwa endapo serikali haitakuwa na fedha za kutekeleza miradi ya maendeleo kwa manufaa ya wananchi wao. Hapa ndipo umuhimu wa ulipaji kodi unapoonekana.

Kimsingi, pamoja na umuhimu wa ulipaji kodi kwa maendeleo, walipakodi wanazo changamoto ambazo wanahitaji kuziwasilisha serikalini kupitia Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ili ziweze kufanyiwa kazi.

Iko hivi: Ulipaji kodi unahusisha wadau wawili yaani TRA na walipakodi. Kutokana na hili, haitawezekana ulipaji kodi ukawa na ufanisi endapo walipakodi hawatatatuliwa changamoto zao kwa wakati. 

Pia, kwa upande wa TRA, hawataweza kukusanya kodi kwa uendelevu mzuri ikiwa walipakodi wao wamesongwa na changamoto lukuki.

Ndiyo maana, kwa kutambua umuhimu wa pande zote kuwa na uhusiano mzuri na kufanikisha ulipaji kodi, TRA wameamua kuitenga siku ya Alhamisi ya kila wiki, nchi nzima, katika ofisi za wilaya na mikoa, kusikiliza kero za wafanyabiashara na walipakodi kwa ujumla.

Na hapa, Meneja Elimu Kwa Mlipakodi TRA, CPA Paul Walalaze, anasema, kutokana na umuhimu wa ulipaji kodi unaozingatia utu, siku ya Alhamisi imetengwa kwa upekee kabisa, kuhakikisha walipakodi wanawasilisha changamoto zao kwa uwazi ili kupata ufafanuzi na ufumbuzi wake.

"Hatuwezi kufanikiwa ukusanyaji kodi kama walipakodi wetu wamesongwa na changamoto. TRA imetenga siku hii ya Alhamisi, wafanyabiashara watoe changamoto zao, maoni na ushauri ili azma ya kukuza maendeleo nchini kwetu ifanikiwe," amesema.

Ameongeza kuwa, "Sasa, siku ya Alhamisi imekuwa jukwaa muhimu kwa walipakodi nchini. Ni siku ambayo walipakodi wanaonana na maofisa mapato kueleza changamoto zao, kupata ufafanuzi wa masuala mbalimbali ya kikodi na kibiashara ili kuweza kufanya shughuli zao katika mazingira mazuri zaidi".

Ikumbukwe kuwa, mwelekeo wa serikali ni kujitegemea kibajeti kwa asilimia kubwa. Mwelekeo huu umejengwa katika misingi kuwa, nchi inajengwa na wananchi wenyewe. 

Pamoja na ukweli kuwa, serikali haitaacha kupokea misaada kutoka kwa wadau na wabia wa maendeleo, lakini misaada hiyo itukute tukiwa katika safari yetu ya kujisimamia na kujitegemea kibajeti kufanikisha miradi ya maendeleo na ya kimkakati.

Ukweli ni kwamba, hatutaweza kufikia dhamira hii njema, endapo walipakodi hawatatatuliwa changamoto zao, ikizingatiwa kuwa walipakodi ndiyo waliobeba hatma ya maendeleo ya nchi kupitia ulipaji kodi.

Kwa kusisitiza hili, CPA Walalaze amesema, "Ewe mlipakodi mwenye changamoto, itumie siku ya Alhamisi kuwasilisha changamoto yako ili ipatiwe ufumbuzi. Utatuzi wa kero za kikodi utawezesha ulipaji kodi kufanyika vizuri na kujenga uhusiano mzuri baina ya Mamlaka na walipakodi wao".

Kwahiyo, mlipakodi hana sababu ya kulalamika, analo jukwaa rasmi la kuwasilisha changamoto zake kwa ufumbuzi zaidi. Utatuzi wa changamoto za walipakodi, utarahisisha ulipaji kodi wa hiari na kuharakisha maendeleo ya wananchi.



Na Pamela Mollel,Arusha

Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) kwa kushirikiana na Serikali ya Ujerumani kupitia GIZ imezindua awamu ya pili ya mpango wa Akili Bandia unaolenga kuwajengea uwezo wananchi kutumia teknolojia ya AI katika kutatua changamoto mbalimbali na kushiriki kikamilifu katika uchumi wa kidijitali

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Naibu Katibu Mkuu wa EAC anayesimamia Miundombinu, Uzalishaji, Jamii na Siasa, Mhe. Aguer Ariik Malueth, amesema mpango huo ni sehemu ya juhudi za Jumuiya kuwaandaa vijana, watafiti na wajasiriamali kutumia fursa zinazotokana na maendeleo ya teknolojia ya Akili Bandia

Amesema awamu hiyo inalenga kuwafikia zaidi ya wananchi 20,000 kutoka nchi wanachama wa EAC kupitia mafunzo ya AI, huku ikiweka mkazo katika kukuza vipaji, ubunifu na utafiti ili Afrika Mashariki iweze kujenga uwezo wa ndani na kushindana katika uchumi wa kidijitali duniani

Kwa upande wake, Mkuu wa Kitengo cha Afrika Mashariki na Kati katika BMZ, Joachim Schmitt, amesema Ujerumani inaona umuhimu wa nchi za EAC kuwa na mwelekeo wa pamoja katika maendeleo ya teknolojia ya AI, akibainisha kuwa uwekezaji mkubwa uliofanyika barani Afrika bado haujasambaa kwa usawa katika nchi zote

Naye Mkurugenzi wa Uvumbuzi na Teknolojia wa Kundi la Equity, Winnie Mangeni, amesema ushirikiano huo utatoa nafasi kwa wanafunzi, watafiti na wabunifu kutengeneza suluhisho zinazotumia AI katika sekta ya fedha na maeneo mengine yenye umuhimu kwa maisha ya wananchi wa Afrika Mashariki

Katika hatua nyingine, waandaaji wametenga Dola za Marekani 50,000 kwa ajili ya kuzisaidia timu zitakazofanya vizuri katika shindano hilo, huku mwaka huu kukiwa na kipengele maalum kinachowaalika wabunifu kutumia AI katika kusaidia kugundua, kuzuia na kukabiliana na milipuko ya magonjwa, ikiwemo Ebola

Mpango huo pia unalenga kuimarisha ufundishaji na utafiti katika vyuo vikuu, kuongeza ujuzi wa kidijitali na kusaidia nchi wanachama kujenga sera zinazofanana kuhusu matumizi ya Akili Bandia, huku ukizingatia usawa wa kijinsia na kuhakikisha teknolojia hiyo inawanufaisha wananchi kwa upana zaidi.











Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Taifa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Wanachama wa Chama hicho katika Maskani Kaka Kisonge, Michenzani Zanzibar, tarehe 11 Agosti, 2026.

Shamra shamra za Mapokezi ya Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Taifa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, baada ya kuwasili Maskani Kaka Kisonge, Michenzani Zanzibar, tarehe 11 Agosti, 2026.







Top News