-Zaidi ya Wataalamu 30 Wanufaika na mafunzo kupitia Mradi wa  Kizuna

📍 Dodoma

Serikali ya Tanzania kupitia Wizara ya Madini na Shirika la Ushirikiano wa Kimataifa la Japan (JICA) zimekubaliana kupanua wigo wa ushirikiano kwa kubainisha maeneo ya kipaumbele yatakayofadhiliwa kupitia JICA kwa msaada wa Serikali ya Japan ikiwemo utafiti wa madini muhimu na mkakati.

Hayo yamebainishwa Juni 25, 2026 jijini Dodoma katika kikao kilicholenga kuimarisha ushirikiano katika maendeleo ya Sekta ya Madini nchini.

Akizungumza katika kikao hicho, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Madini Msafiri Mbibo amesema ushirikiano na taasisi hiyo ni wa muda mrefu ambao kupitia JICA zaidi ya wataalamu 30 wa Sekta ya Madini wamepatiwa mafunzo nchini Japan yaliyowajengea uwezo na kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu ya Wizara na taasisi zake na kueleza kwamba, ushirikiano huo utaendelea kuimarishwa kwa manufaa ya Tanzania na Japan.

Kwa upande wake, Mwakilishi Mkazi wa JICA nchini Tanzania, Dkt. Katsuyika Kuge, amesema pamoja na utekelezaji wa Mradi wa Kizuna unaojenga uwezo wa wataalamu wa sekta hiyo, JICA inapanga kupanua ushirikiano katika maeneo ya utafiti wa madini muhimu na madini mkakati, ikiwemo shaba, kinywe (graphite), beryllium na madini adimu ya Heavy Rare Earth Elements (Heavy REE). 

Aidha, Dkt. amefafanua kuwa, kwa kuanzingatia vipaumbele vya JICA, kwa kuanzia,  kipaumbele  cha utafiti kitajikita kwenye eneo la madini kinywe na beryllium.

‘’ Ninaipongeza Serikali ya Tanzania kwa usimamizi mzuri wa Sekta ya Madini, pamoja na utekelezaji wa mradi wa Kizuna unaowajengea uwezo watalaam wa Sekta ya madini, JICA inapanga kupanua ushirikiano katika maeneo ya utafiti wa madini muhimu na mkakati,’’ amesema Dkt.Kuge.






-Uchumi wa Bluu Kunufaika na Elimu ya Ubaharia

Na Mwandishi Wetu, Kigoma

Waziri wa Uchukuzi, Profesa Makame Mnyaa Mbarawa, amesema Serikali itaendelea kukiunga mkono Chuo cha Bahari Dar es Salaam (DMI) katika jitihada zake za kuanzisha kozi ya awali ya ubaharia itakayowawezesha vijana wengi zaidi wa Kitanzania kupata elimu ya sekta hiyo na kushiriki kikamilifu katika kukuza uchumi wa bluu.

Profesa Mbarawa ametoa kauli hiyo alipotembelea banda la DMI katika kilele cha Maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani yaliyofanyika mkoani Kigoma, ambapo alieleza kuwa kozi hiyo ni suluhisho kwa vijana wengi wenye ndoto za kuwa mabaharia lakini ambao hawakupata nafasi ya kusoma masomo ya sayansi yanayohitajika kujiunga na taaluma hiyo.

Alisema DMI imebuni mpango huo mahsusi ili kuwapa vijana hao fursa ya kupata msingi wa masomo muhimu yatakayowawezesha kuendelea na mafunzo ya ubaharia na hatimaye kuingia katika soko la ajira la sekta ya usafiri wa majini.

“DMI inafanya kazi kubwa ya kuangalia namna ya kuwawezesha vijana wengi zaidi kupata fursa za elimu ya ubaharia. Kozi hii ya awali itawasaidia wale ambao hawakusoma masomo ya sayansi kupata msingi unaohitajika na hatimaye kujiunga na mafunzo ya ubaharia,” alisema Profesa Mbarawa.

Alibainisha kuwa hatua hiyo ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kuongeza idadi ya mabaharia wenye ujuzi na sifa zinazotambulika kitaifa na kimataifa, huku ikilenga kuongeza ushiriki wa Watanzania katika ajira za sekta ya bahari na usafiri wa majini duniani.

Waziri huyo pia alimpongeza Mkuu wa Chuo cha DMI, Profesa Tumaini Gurumo, kwa ubunifu na juhudi zake za kuendeleza programu mbalimbali za mafunzo zinazowawezesha mabaharia wa Tanzania kufikia viwango vya kimataifa vinavyohitajika katika sekta ya usafiri wa majini.

“Tunakipongeza DMI kwa juhudi zake za kubuni na kuendeleza mafunzo yanayowawezesha mabaharia wetu kuwa na sifa zinazokubalika kimataifa. Mabaharia wanazunguka dunia nzima, hivyo ni lazima waandaliwe kwa viwango vinavyokidhi mahitaji ya sekta ya kimataifa,” alisema Profesa Mbarawa.

Kwa upande wake, Mkuu wa Chuo cha DMI, Profesa Tumaini Gurumo, ameishukuru Serikali kupitia Wizara ya Uchukuzi kwa kuendelea kukiunga mkono chuo hicho katika kuzalisha wataalamu wenye tija na ushindani katika soko la ajira la ndani na nje ya nchi.

Profesa Gurumo alisema kutokana na asili ya kazi ya ubaharia inayowafanya mabaharia kufanya kazi na kusafiri katika mataifa mbalimbali duniani, ni muhimu kwao kupata elimu na stadi zinazotambulika kimataifa ili waweze kushindana kwa ufanisi katika soko la ajira la dunia.

Aliongeza kuwa DMI itaendelea kupanua na kuboresha mafunzo ya bahari ili kuhakikisha vijana wengi zaidi wanapata elimu na ujuzi unaohitajika kwa taifa kunufaika na fursa zilizopo katika uchumi wa bluu na sekta ya usafiri wa majini.

Maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani yamewakutanisha wadau mbalimbali wa sekta ya bahari na usafiri wa majini kwa lengo la kutambua na kuthamini mchango mkubwa wa mabaharia katika kukuza biashara, uchumi na maendeleo ya jamii duniani.



Matukio ya picha ya Waziri Profesa Mbarawa katika Banda la DMI,Kigoma

Na Janeth Raphael-MichuziTv


Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) limeahidi kuchangia fedha kwa ajili ya kuimarisha huduma za upandikizaji figo na uroto (selimundu) katika Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH), ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za Serikali za kuboresha huduma za afya nchini kuelekea maadhimisho ya miaka 10 ya hospitali hiyo yanayotarajiwa kufanyika Julai 15, 2026.

Akizungumza wakati wa ziara ya wahariri wa vyombo mbalimballi vya habari nchini katika hospitali hiyo jijini Dodoma, Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania, Deodatus Balile, amesema mchango huo unalenga kusaidia wagonjwa wasiokuwa na uwezo wa kugharamia matibabu ya kibingwa yanayotolewa na hospitali hiyo.

Balile amesema huduma za kibingwa zinazopatikana BMH zimekuwa mkombozi kwa Watanzania wengi kutokana na ubora wake na gharama nafuu ikilinganishwa na matibabu yanayopatikana nje ya nchi.

“Hakuna mtu ambaye hapendi kupata huduma bora kwa gharama nafuu. Sisi kama wahariri tumeona ni muhimu kuunga mkono juhudi hizi kwa kuchangia ili kuwasaidia wale wasiokuwa na uwezo wa kumudu gharama za matibabu,” amessema Balile.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa BMH, Dkt. Abdalla Baja, amesema hospitali hiyo imeendelea kupanua wigo wa huduma za kibingwa na ubingwa bobezi, ikiwa na madaktari bingwa bobezi 18 pamoja na madaktari bingwa 20 wanaotoa huduma mbalimbali za matibabu ya hali ya juu.

Amesema mbali na huduma za upandikizaji figo na uroto, hospitali hiyo imefikia hatua ya kutoa huduma za upandikizaji wa uume kwa wagonjwa wenye changamoto zinazohitaji tiba hiyo maalumu.

Dkt. Baja aliongeza kuwa BMH imeandika historia kwa kuwa hospitali ya kwanza Afrika Mashariki kufanya upandikizaji wa uroto (selimundu), hatua ambayo imeifanya kuwa kituo muhimu cha rufaa kwa wagonjwa kutoka nchi mbalimbali za Afrika Mashariki na Kati.

Naye Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Damu, Dkt. Happiness Joseph Igogo, alisema hospitali hiyo imejipanga kuongeza idadi ya wagonjwa wanaopatiwa huduma za upandikizaji wa uroto kutoka wagonjwa 10 hadi 20 kwa mwaka.

Amesema mafanikio ya huduma hiyo yamechangia kwa kiasi kikubwa kupunguza vifo vinavyotokana na ugonjwa wa selimundu na kutoa matumaini mapya kwa wagonjwa wengi.

Kwa upande wake, Meneja wa Mkoa wa Dodoma wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF), Irene Kataraihya, alisema taasisi hiyo imejipanga kushiriki kikamilifu katika mfuko maalumu wa kusaidia huduma hizo muhimu ili kuendelea kuokoa maisha ya Watanzania.

Akizungumzia huduma za figo, Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Ndani na Figo, Dk. Ayubu Masamba, amesema huduma za upandikizaji figo zinazotolewa BMH zimepunguza kwa kiwango kikubwa idadi ya wagonjwa waliokuwa wakisafiri nje ya nchi kutafuta matibabu hayo.

Amesema hatua hiyo imechangia kupunguza gharama kubwa za matibabu kwa wagonjwa na familia zao huku ikiimarisha upatikanaji wa huduma za kibingwa ndani ya Tanzania.

Maadhimisho ya miaka 10 ya Hospitali ya Benjamin Mkapa yanatarajiwa kuwa fursa ya kuonesha mafanikio makubwa yaliyopatikana katika utoaji wa huduma za afya za kibingwa na ubingwa bobezi, huku hospitali hiyo ikiendelea kuwa kinara wa huduma za kisasa za matibabu nchini na katika ukanda wa Afrika Mashariki.



-Lumbila Wapata Umeme kwa Mara ya Kwanza Tangu Uhuru

-Giza la Miaka 60 Lamalizika Wilayani Ludewa


Ludewa, Njombe📍

Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kwa kushirikiana na mkandarasi; Shirika la Uzalishaji Mali JKT (SUMA JKT) leo, tarehe 25 Juni, 2026 kwa mara ya kwanza wamewasha umeme katika kitongoji cha Lumbila katika Halmashauri ya wilaya ya Ludewa ambapo eneo hilo lilikuwa halijapa umeme tangu Tanzania ipate uhuru wake 9 Desemba, mwaka 1961.

Akiongoza hafla hiyo ya kuwasha umeme kwa mara ya kwanza, Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB); Bodi inayoisimamia REA; Mhe. Balozi na Meja Jenerali Mstaafu, Jacob Kingu alisema utekelezaji wa mradi huo ni ushahidi wa dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha huduma ya umeme inawafikia Watanzania wote bila kujali umbali na changamoto za kijiografia.

Eneo hili lilikuwa halijawahi kupata umeme kwa zaidi ya miaka 60 tangu Tanzania ipate uhuru wake mwaka 1961. Hafla hiyo ya kuwasha umeme kwa mara ya kwanza katika Kitongoji cha Lumbila imefanyika katika Kanisa Katoliki la Kitongoji cha Lumbila, hatua iliyopokelewa kwa furaha kubwa na Wananchi wa eneo hilo.

Awali kabla ya kumkaribisha Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB); Mheshimiwa Balozi na Meja Jenerali Mstaafu, Jacob Kingu, Mhandisi, Thomas Mmbaga amaye alimwakilisha Mkurugenzi wa Umeme Vijijini alisema, Mradi wa kusambaza umeme kwenye vitongoji sita vya mwambao wa Ziwa Nyasa umetumia gharama ya Shilingi bilioni 3.124 na kuongeza kuwa hadi sasa mradi umefikia asilimia 67, ambapo vitongoji 3 kati ya 6 vya mwambao wa Ziwa Nyasa vimeshawashiwa umeme.

Mhandisi Mmbaga ameongeza kuwa Mradi unahusisha ujenzi wa kilomita 36.6 za njia za msongo wa kati na kilomita 15.1 za msongo mdogo.

“Mradi unatarajiwa kuwafikia wateja 151 wa njia moja (single-phase) na wateja 9 wa njia tatu (three-phase). Tayari kaya zaidi ya 23 zimeomba kuunganishiwa”. Amekaririwa, Mhandisi, Mmbaga.

Naye, Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya SUMA JKT Company Ltd, Meja James Simon Mwame, alisema utekelezaji wa Mradi huo ulikuwa na changamoto kubwa kutokana na mazingira ya mwambao wa Ziwa Nyasa, lakini juhudi za wataalam na wafanyakazi wa kampuni hiyo zimewezesha ndoto ya Wananchi kupata umeme kutimia.

Meja Mwame alisema SUMA JKT ni kampuni inayojihusisha na ujenzi na usambazaji wa miundombinu ya umeme nchini, na kwa Mkoa wa Njombe kampuni hiyo inatekeleza miradi ya usambazaji umeme katika wilaya za Ludewa na Makete.

Ziara ya viongozi (ikiongozwa na Mwenyekiti wa Bodi ya REA, Balozi Jacob Kingu) ilihusisha safari ya majini kwa boti ya takribani kilomita 11 kutoka Pwani ya Matema (Kyela, Mbeya) hadi Ludewa kutokana na ugumu wa kijiografia na miundombinu ya usafirishaji wa vifaa.

Mwananchi wa eneo hilo, Bakari Gowele, amebainisha kuwa umeme huo utasaidia sana sekta ya uvuvi kwani sasa wataweza kutengeneza barafu na kuhifadhi samaki kwa muda mrefu ili kuwafikisha kwenye masoko ya mbali wakiwa katika ubora wa hali ya juu.








-Asilimia 80 ya Mizigo Inaingia Tanzania Kwa Njia ya Maji

NA MWANDISHI WETU, KIGOMA

WAZIRI wa Uchukuzi, Profesa Makame Mnyaa Mbarawa, amesema mabaharia ni nguzo muhimu ya usafirishaji duniani na walinzi wakuu wa mnyororo wa biashara na uchumi, hivyo wanapaswa kuendelea kupewa mazingira bora ya kazi, mafunzo na fursa za maendeleo ili kuongeza mchango wao katika uchumi wa taifa.

Profesa Mbarawa ametoa kauli hiyo wakati wa kilele cha Maadhimisho ya 16  Siku ya Mabaharia Duniani yaliyofanyika mkoani Kigoma.

Alisema zaidi ya asilimia 80 ya biashara ya dunia husafirishwa kwa njia ya maji, jambo linalowafanya mabaharia kuwa mhimili muhimu wa uchumi wa kimataifa licha ya kukabiliwa na changamoto mbalimbali wanazokutana nazo ikiwemo kukaa muda mrefu baharini, kutengana na familia zao, mazingira magumu ya kazi na hatari za kiusalama, bado wanaendelea kutekeleza majukumu yao kwa weledi na kujitolea.

“Mabaharia ndio uti wa mgongo wa sekta ya usafirishaji duniani. Kazi yao inahakikisha bidhaa muhimu zinafika kwa wakati na uchumi wa dunia unaendelea kuzunguka. Tunawapongeza kwa moyo wao wa kujitolea na uzalendo,” alisema.

Amesema kauli mbiu ya maadhimisho hayo inapaswa kutekelezwa kwa vitendo kupitia sera madhubuti, utoaji wa mafunzo ya kisasa na kuimarisha ushirikiano wa kimataifa ili kuhakikisha sekta ya usafiri majini inakua sambamba na mahitaji ya dunia ya sasa.

“Mabaharia ni mhimili mkubwa wa uchumi wa dunia. Tunapaswa kuhakikisha wanapatiwa mafunzo yanayoendana na mabadiliko ya teknolojia na mazingira ya kazi ili waweze kukabiliana na kasi ya mabadiliko yanayotokea duniani,” amesema Profesa Mbarawa.

Ameeleza kuwa maadhimisho ya mwaka huu yanaenda sambamba na juhudi za Serikali za kuongeza uwekezaji katika shughuli za usafirishaji na uchumi wa bluu, hatua ambayo imeendelea kufungua fursa nyingi za ajira kwa vijana na wanawake.

Kwa mujibu wa Waziri huyo, ongezeko la ajira katika sekta ya usafiri majini linaendana na malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayolenga kukuza uchumi, kuongeza uzalishaji na kuboresha maisha ya wananchi.

Aidha, amesema Tanzania na Uganda zimeingia katika makubaliano ya ushirikiano wa shughuli za utafutaji na uokoaji majini, huku akieleza kuwa utekelezaji wa sheria na mifumo ya utafutaji na uokoaji utasaidia kuimarisha usalama wa mabaharia, abiria na vyombo vya usafiri majini.

Profesa Mbarawa amewataka mabaharia kuendelea kuwa waadilifu, kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za kazi pamoja na kutoa taarifa kwa mamlaka husika pindi wanapobaini changamoto zinazoweza kuhatarisha usalama wa vyombo na watu.

Amesema maadhimisho hayo yamekuwa jukwaa muhimu la utoaji elimu, kubadilishana uzoefu na kutoa maelekezo yatakayosaidia kukuza sekta ya usafiri wa majini nchini.

Katika hatua nyingine, ameliagiza Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC) kuharakisha utekelezaji wa mikakati ya kuwatafutia mabaharia wa Tanzania fursa zaidi za ajira katika soko la kimataifa, huku akisisitiza umuhimu wa kuwapa wanawake kipaumbele katika ajira za sekta hiyo.

Pia ameitaka TASAC kukamilisha kanzidata ya mabaharia nchini pamoja na kufanya tathmini ya mifumo ya maslahi yao ili kuhakikisha ustawi wa mabaharia unaimarishwa na changamoto zao zinapatiwa ufumbuzi kwa wakati.

Vilevile, ameshauri TASAC kuendelea kufanya mazungumzo na wamiliki wa meli mbalimbali ili waweze kufungua ofisi zao nchini Tanzania hatua itakayorahisisha upatikanaji wa ajira kwa mabaharia wa Kitanzania na kuongeza ushindani wao katika soko la kimataifa.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa TASAC Mohamed Salum amesema kuwa TASAC imesaini mikataba mbalimbali ya Kimataifa hatua ambayo itasaidia kuongeza uwigo wa ajira kwa mabaharia.

Amesema kuwa Serikali imefanya uwekazaji katika bandari ambapo fursa zimeongezeka kwa mabaharia pamoja kuendelea kuratibu katika mfumo kwa mabaharia kuwa kwenye mfumo huo.

Aidha amesongeza kuwa TASAC imenunua Boti za uokozi ili kuhakikisha wananchi na mabaharia wanakuwa salama wakati wote na wakipata majanga wanaokolewa.

Waziri wa Uchukuzi Profesa Makame Mnyaa Mbarawa (MB)akifunga maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani   yaliyofanyika Viwanja vya Center mjini Kigoma
Mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa ,Mkuu wa Wilaya ya Kigoma Dkt.Rashid Chuachua akizungumza wakati wa kumkaribisha mgeni rasmi katika Kilele cha maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani   yaliyofanyika Viwanja vya Center mjini Kigoma.
Mwenyekiti wa Bodi ya TASAC Nah.Mussa Mandia akitoa maelezo katika kilele cha  maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani   yaliyofanyika Viwanja vya Center mjini Kigoma.
Mkurugenzi Mkuu wa TASAC Mohamed Salum akitoa maelezo kuhusiana na umhimu wa mabaharia  katika maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani   yaliyofanyika Viwanja vya Center mjini Kigoma.
Mkuu wa Chuo cha DMI Profesa Tumain Gurumo akizungumza katika kilele cha maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani   yaliyofanyika Viwanja vya Center mjini Kigoma.


Picha za makundi mbalimbali katika kilele katika maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani   yaliyofanyika Viwanja vya Center mjini Kigoma.


Timu ya wataalamu kutoka Ofisi ya Rais–UTUMISHI kwa kushirikiana na Watumishi Housing Investment imefanya ziara ya ukaguzi wa miradi ya ujenzi wa nyumba za watumishi awamu ya pili katika Wilaya ya Dodoma, ikiwa ni sehemu ya kuhakikisha miradi hiyo inatekelezwa kwa kuzingatia ubora, thamani ya fedha na ratiba iliyopangwa.

Ziara hiyo imeongozwa na Mkurugenzi wa Kitengo cha Ufuatiliaji na Tathmini, Bw. Patrick Allute, ambaye amesema Serikali imeendelea kuimarisha mazingira ya kazi na makazi ya watumishi wa umma ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma kwa wananchi.

Bw. Allute amesisitiza umuhimu wa usimamizi madhubuti wa miradi, matumizi sahihi ya rasilimali za umma na ukamilishaji wa kazi kwa wakati huku viwango vya ubora vikizingatiwa. Aidha, ametoa maelekezo kwa wasimamizi wa miradi na wakandarasi kushughulikia kwa haraka changamoto zilizobainika ili kuhakikisha malengo ya miradi hiyo yanafikiwa kama ilivyopangwa.

Ziara hiyo imekuwa sehemu ya juhudi za Serikali za kuimarisha ufuatiliaji wa miradi ya maendeleo ili kuhakikisha uwekezaji unaofanywa unaleta matokeo yaliyokusudiwa kwa manufaa ya watumishi wa umma na wananchi kwa ujumla.

Katika ukaguzi huo, timu imetembelea miradi ya ujenzi wa nyumba za watumishi katika Kituo cha Afya Hombolo, Shule ya Sekondari Mtemichiloloma, Kituo cha Afya Mkonze na Shule ya Sekondari Bihawana, ambapo imejionea maendeleo ya utekelezaji wa miradi hiyo na imefanya majadiliano na wasimamizi pamoja na wakandarasi kuhusu hatua zilizofikiwa na changamoto zinazojitokeza.



Balozi Mobhare Matinyi akimwonesha Afisa Mtendaji Mkuu wa kampuni ya Géant Electronics, Abdelkrim Mebarkia, vivutio vya utalii na fursa za uwekezaji nchini Tanzania kwenye banda la Tanzania katika Maonesho ya 57 ya Biashara ya Kimataifa ya Algiers (FIA) yanayoendelea nchini Algeria.

Balozi Mobhare Matinyi akipata maelezo ya kitaalam kuhusu uzalishaji wa nyasi bandia zinazotambuliwa na FIFA kutoka kwa Mkurugenzi wa Mauzo na Masoko wa kampuni ya Tapidor ya Algeria, Yahia Ballalou (kulia). Kushoto ni Bounouare Adel, Mkurugenzi wa Uhusiano wa Kimataifa wa Tapidor.
Balozi Mobhare Matinyi akizungumza na washiriki wa taasisi za Serikali ya Tanzania, Robert Mtendawema (kushoto) ambaye ni Meneja wa Tehama na Takwimu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea Tanzania (TFRA), Gilbert Lyimo (wa pili kulia) ambaye ni Kaimu Mhasibu Mkuu wa Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) na Omary Mafita (kulia), Afisa Hesabu Mkuu wa WRRB.


Kampuni za Algeria zinazojishughulisha na uzalishaji wa bidhaa mbalimbali zikiwemo za viwandani na kilimo zinatafuta wabia wa kufanya nazo biashara ya mazao na uwekezaji katika sekta ya viwanda nchini Tanzania.

Kampuni hizo zilizovutiwa kushirikiana na Tanzania zinashiriki katika Maonesho ya 57 ya Biashara ya Kimataifa ya Algiers (FIA) yaliyofunguliwa na Rais Abdelmadjid Tebboune wa Algeria mnamo tarehe 22 Juni, 2026, katika Kituo cha Maonesho cha Shirika la Maonesho na Biashara ya Nje la Algeria (SAFEX).

Maonesho haya ndiyo makubwa zaidi miongoni mwa maonesho ya kimataifa nchini Algeria yakiwa yanazishirikisha jumla ya kampuni 731 zinazojumuisha 549 za Algeria kutoka katika kila sekta na kampuni za kigeni 202 kutoka nchi 36 zikiwemo 16 za Afrika.

Akizungumza katika siku ya pili ya maonesho kwenye banda la Tanzania, Balozi Mobhare Matinyi alizitaja kampuni hizo zinazotafuta wabia nchini kuwa ni GISB inayotaka kuuza vifaa vya umeme na kutengeneza nyaya za umeme kwa kutumia shaba ya Tanzania na GETEX inayotaka kununua katani na pamba na kuwekeza katika kiwanda cha kutengeneza bidhaa za ngozi.

“Afisa Mtendaji Mkuu wa GISB, Dkt. Mohamed Khelifa, anakuja tena nchini mwezi Julai baada ya ziara yake ya kwanza mwezi Mei 2026 wakati watendaji wakuu wa kampuni tatu tanzu za GETEX wamepanga kuja nchini mwezi Oktoba 2026 kutembelea Kiwanda cha Kimataifa cha Bidhaa za Ngozi cha Kilimanjaro (KLICL) ili kuona namna ya kushirikiana”, alisema Balozi Matinyi.

Kampuni zingine ni Tapidor inayotengeneza na kuuza mazulia pamoja na nyasi bandia za viwanja vya soka, Optimaflex ya magodoro, Géant Electronics ya bidhaa za umeme, Bellat ya kusindika nyama na ujenzi wa makaazi pamoja na SARL CPC inayotaka kununua dagaa wa baharini na samaki aina ya jodari ambayo Meneja Mkuu wake, Samir Benhamada, ataitembelea Kampuni ya Uvuvi Zanzibar (ZAFICO) mwezi Julai 2026.

Balozi Matinyi aliongeza zaidi kuwa: “Kampuni zingine za Algeria zinataka kununua bidhaa za kahawa, korosho, ndizi, maharage ya soya, mchele, maziwa ya unga na nyama za ng’ombe, mbuzi na kondoo ambazo huliwa kwa wingi nchini Algeria,” akitolea mfano wa sikukuu ya Idi Al-Adha ambapo Serikali ya Algeria iliingiza kondoo milioni moja kutoka nje ya nchi.

Katika maonesho haya Tanzania inatangaza fahari yake ya utalii wa hifadhi, fukwe za bahari, milima, historia ya kale na utamaduni pamoja na fursa za uwekezaji katika sekta za madini, viwanda, kilimo, nishati na usafirishaji na vilevile mazao ya chakula na biashara.

Mbali ya Ubalozi, taasisi mbili za Serikali ya Tanzania zinazoshiriki ni Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea Tanzania (TFRA) inayowakilishwa na Meneja wa Tehama na Takwimu, Robert Mtendawema; na Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) inayowakilishwa na Kaimu Mhasibu Mkuu Gilbert Lyimo na Afisa Hesabu Mkuu Omary Mafita.

Imetolewa na Ubalozi wa Tanzania,

Algiers, Juni 24, 2026.


Na Karama Kenyunko Michuzi Tv
SERIKALI ya Tanzania imesema iko tayari kuongeza uzalishaji wa bidhaa na kutumia fursa ya soko la China kufuatia hatua ya taifa hilo kuondoa ushuru kwa bidhaa zinazotoka nchi za Afrika.

Balozi wa Tanzania nchini China, Dkt. Suleiman Haji Suleiman, amesema hayo leo Juni 25,2026 jijini Dar es Salaam wakati akizungungumza na waandishi wa habari kuhusu ushirikiano wa Tanzania na China ulipofikia na fursa mbali mbali zitokanazo na ushirikiano huo.

Amesema hatua hiyo inaipa Tanzania nafasi ya kuuza zaidi bidhaa zake katika soko la China bila kutozwa ushuru, mradi bidhaa hizo zikidhi sheria za biashara za China na zile za Jumuiya ya Umoja wa Mataifa.

Akizungumzia mwenendo wa biashara kati ya Tanzania na China, Balozi Suleiman alisema kati ya mwaka 2021 na 2025 thamani ya biashara kati ya nchi hizo mbili imefikia Dola za Marekani bilioni 23.2.

Alisema kati ya kiasi hicho, Tanzania iliuza bidhaa zenye thamani ya Dola za Marekani bilioni 1.8 pekee, sawa na asilimia nane, huku bidhaa zilizoagizwa kutoka China zikifikia Dola za Marekani bilioni 21.3.

Alieleza kuwa pengo hilo linasababishwa na uzalishaji mdogo pamoja na kuendelea kuuza bidhaa ghafi bila kuziongezea thamani kabla ya kuzipeleka katika masoko ya kimataifa.

“Kwa mfano tunapeleka korosho ghafi China, wao wanazifungasha vizuri na kuziongezea thamani, kisha bidhaa hizo zinarejea tena sokoni. Kuna haja ya sisi kuongeza thamani bidhaa zetu hapa nchini kabla ya kuzipeleka nje,” alisema.

Balozi Suleiman alisema ubalozi unaendelea kutafuta fursa zaidi za uwekezaji kutoka China, hususan katika sekta za teknolojia, viwanda na upatikanaji wa mitambo ya kisasa ya uzalishaji ili kusaidia azma ya serikali ya kukuza uchumi wa viwanda.

Alisema makampuni mbalimbali kutoka China tayari yameonesha nia ya kuwekeza nchini, hatua ambayo inatarajiwa kuongeza ajira kwa Watanzania na kukuza uzalishaji wa ndani.

Wakati huo huo, Ubalozi wa Tanzania nchini China umetangaza kufungua kliniki maalumu ya biashara katika Maonesho ya 49 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba) kwa lengo la kutoa ushauri wa moja kwa moja kwa Watanzania wanaotaka kuuza bidhaa katika soko la China au kuagiza mitambo kutoka nchini humo.

Alisema wataalamu kutoka ubalozini watakuwepo muda wote wa maonesho hayo kutoa elimu kuhusu bidhaa zinazohitajika katika soko la China, namna ya kusafirisha bidhaa, kupata vibali pamoja na fursa za uwekezaji na ununuzi wa mitambo ya viwandani.

“Lengo kuu ni kutoa huduma za ushauri kwa Watanzania kuelewa maana halisi ya soko la China, bidhaa gani unaweza kuzipeleka, namna ya kuzipeleka, sheria gani zinahitajika na namna ya kuomba vibali mbalimbali,” alisema.

Aidha, alisema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan imeendelea kusukuma mbele diplomasia ya uchumi kwa lengo la kuongeza uzalishaji, ajira na mapato ya taifa kupitia biashara na uwekezaji.

“China siyo tu soko la bidhaa zetu, bali pia ni chanzo kikubwa cha teknolojia na mitambo inayoweza kusaidia maendeleo ya viwanda vyetu na kuongeza thamani ya bidhaa zinazozalishwa nchini,” alisema.









Paris, Ufaransa
CHUO cha Dhow Countries Music Academy (DCMA) cha Zanzibar kimeandika historia baada ya kutangazwa mshindi wa Tuzo ya 21 ya UNESCO-Sharjah Prize for Arab Culture, katika hafla iliyofanyika Makao Makuu ya UNESCO jijini Paris, Ufaransa. Chuo hicho kimetunukiwa tuzo hiyo kutokana na mchango wake mkubwa katika kuhifadhi, kufundisha na kuendeleza urithi wa muziki wa taarab na tamaduni za ukanda wa Bahari ya Hindi na Kiarabu.

Mwakilishi wa chuo hicho, Bi. Haldah Am Al-Kanaan, alikuwepo Paris kupokea tuzo hiyo kwa niaba ya taasisi. DCMA ni chuo pekee cha muziki Zanzibar kinachojikita katika kufundisha ala za asili na mitindo ya muziki wa jadi ikiwemo taarab, kidumbak na ngoma, huku kikileta pamoja wanafunzi kutoka mataifa mbalimbali na rika tofauti.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mkurugenzi Mkuu wa UNESCO, Profesa Khaled El-Enany, alikipongeza chuo hicho kwa ubunifu wake katika kuhifadhi na kuendeleza urithi wa muziki wa Kiarabu na Kiswahili. Alisema majaji kutoka mabara mbalimbali walivutiwa na namna DCMA ilivyoweza kutumia muziki kama daraja la kuunganisha tamaduni tofauti, pamoja na mazingira yake ya kujifunzia yanayowakutanisha wanafunzi kutoka sehemu mbalimbali duniani.

Kwa upande wake, uongozi wa DCMA ulieleza kuwa tuzo hiyo ni heshima kubwa kwa Zanzibar na Tanzania, na kwamba itakuwa chachu ya kuongeza juhudi katika kulinda na kuendeleza urithi wa taarab na muziki wa jadi kwa vizazi vijavyo.

Hafla hiyo pia ilihudhuriwa na Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Ufaransa na Mwakilishi wa Kudumu katika UNESCO, Balozi Saidi Othman Yakubu, ambaye alishuhudia tukio hilo la kihistoria na kuwapongeza washindi kwa kuitangaza vyema Tanzania kupitia sanaa na utamaduni katika jukwaa la kimataifa.

Tuzo ya UNESCO-Sharjah Prize for Arab Culture, iliyoanzishwa mwaka 1998 kwa ushirikiano kati ya UNESCO na Serikali ya Sharjah, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE), hutolewa kila mwaka kwa watu binafsi au taasisi zilizotoa mchango wa kipekee katika kuendeleza na kutangaza utamaduni wa Kiarabu na kuimarisha mazungumzo ya tamaduni duniani. Katika toleo la mwaka huu, DCMA ilitangazwa mshindi pamoja na mwanamuziki na mjasiriamali wa utamaduni kutoka Morocco, Brahim El Mazned.

Na, Mwandishi Wetu – Dodoma

SERIKALI imesema itaendelea kuimarisha mifumo ya usimamizi wa maafa nchini ili kupunguza madhara yanayosababishwa na majanga mbalimbali ambayo yamekuwa yakigharimu maisha ya watu, kuharibu mali na kurudisha nyuma maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Kauli hiyo imetolewa hii leo 25 Juni, 2026 na Naibu Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Dkt. James Kilabuko, wakati akifunga Jukwaa la Wadau wa Usimamizi wa Maafa lililojadili Rasimu ya Mpango wa Taifa wa Dharura wa Kuzuia na Kukabiliana na Madhara ya El Niño Jijini Dodoma.

Amesema Tanzania imeendelea kukabiliwa na matukio ya maafa yanayosababisha athari kubwa kwa wananchi na uchumi wa Taifa, hali inayolazimu kuwepo kwa maandalizi madhubuti ya kukabiliana na changamoto hizo kabla hazijatokea.

“Nchi yetu imekuwa ikishuhudia matukio ya majanga ambayo yamekuwa yakisababisha maafa na kuathiri mfumo wa kawaida wa maisha ya jamii. Majanga hayo yamesababisha vifo, ulemavu wa kudumu, upotevu wa mali na uharibifu wa miundombinu,” amesema Dkt. Kilabuko.

Amesema kufuatia taarifa ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) ya Aprili 28, 2026 kuhusu uwezekano wa kujitokeza kwa hali ya El Niño, Ofisi ya Waziri Mkuu imeandaa Rasimu ya Mpango wa Taifa wa Dharura kwa ajili ya kuzuia na kukabiliana na madhara yanayoweza kutokea kuanzia Agosti 2026 hadi Juni 2027.

Kwa mujibu wa Dkt. Kilabuko, rasimu hiyo imejadiliwa na wadau mbalimbali ili kuiboresha kwa kuzingatia uzoefu uliopatikana wakati wa matukio ya El Niño yaliyowahi kutokea nchini, hususan ya mwaka 2023/2024.

Amesema ushirikishwaji wa wadau ni hatua muhimu itakayoiwezesha Serikali kuwa na mpango shirikishi na unaotekelezeka katika kuzuia, kujiandaa, kukabiliana na kurejesha hali endapo maafa yatatokea.

“Ni vema kushiriki kikamilifu na kutoa maoni yetu huku tukijielekeza kwenye athari tarajiwa na hatua za kuchukua ili kuwa na mpango thabiti utakaoiwezesha Serikali na wadau kuchukua hatua stahiki za kuzuia au kupunguza madhara,” amesema.

Aidha, ameeleza imani yake kuwa jukwaa hilo litatoa mchango mkubwa katika kuimarisha ufanisi wa usimamizi wa maafa nchini na kuongeza uwezo wa taasisi mbalimbali kukabiliana na changamoto za majanga.

Dkt. Kilabuko amesisitiza kuwa usimamizi wa maafa haupaswi kuonekana kama jukumu la taasisi chache pekee, bali unapaswa kujumuishwa katika mipango ya maendeleo na utekelezaji wa shughuli za kila siku za wizara, taasisi na mamlaka za serikali za mitaa.

Amesema hatua hiyo itasaidia kujenga jamii yenye uwezo wa kuhimili majanga na kulinda maendeleo yaliyopatikana nchini dhidi ya athari zinazoweza kusababishwa na hali ya El Niño na majanga mengine.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu Brigedia Jenerali Hosea Ndagala amesema kuwa,Jukwaa hilo ni muhimu na lipo kisheria hivyo litumike kwa manufaa na kuzingatia umuhimu wake.

Aidha alitumia nafasi hiyo kuzikumbusha kamati za maafa ngazi zote kuendelea kujiandaa na kukabiliana na maafa pindi yanapotokea kwa kuendelea kuweka mipango madhubuti ili kupunguza madhara yanayoweza kujitokeza hasa yale ya uharibifu wa miundombinu na kuepuka madhara mengine kwa jamii na Taifa kwa Ujumla.










Top News