Na Janeth Raphael MichuziTv - Bungeni Dodoma 

Soko la ajira nchini Tanzania limeendelea kuimarika, baada ya kiwango cha ukosefu wa ajira kushuka hadi asilimia 6.2 mwaka 2024, ikilinganishwa na asilimia 8.7 iliyorekodiwa mwaka 2020/21.

Hayo yamebainishwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo, wakati akiwasilisha Bungeni Taarifa ya Hali ya Uchumi wa Taifa kwa mwaka 2025 pamoja na Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa mwaka 2026/27.

Profesa Mkumbo amesema hali hiyo ni ishara ya kuimarika kwa mazingira ya biashara, uwekezaji na uzalishaji nchini, hali inayochochea ongezeko la nafasi za ajira katika sekta mbalimbali.

Kwa mujibu wa takwimu hizo, kasi ya ukuaji wa ajira pia imepanda kwa kiwango kikubwa, ambapo wastani wa ukuaji wa ajira kwa mwaka umefikia asilimia 7.8 mwaka 2024, kutoka asilimia 2.3 mwaka 2020/21.

Aidha, nguvu kazi nchini imeongezeka na kufikia watu milioni 27.3, sawa na asilimia 73.2 ya wananchi wote wenye uwezo wa kufanya kazi, ikilinganishwa na asilimia 72.1 ya mwaka 2020/21.

Kati ya nguvu kazi hiyo, takriban watu milioni 25.6 wanajishughulisha na shughuli za kiuchumi zinazowaingizia kipato, hali inayoonyesha ushiriki mpana wa wananchi katika uzalishaji.

Kwa upande wa sekta, kilimo kinaendelea kuwa mwajiri mkubwa zaidi nchini kwa asilimia 54.2, kikifuatiwa na sekta ya huduma yenye asilimia 35.5, huku sekta ya viwanda ikichukua asilimia 10.3 ya ajira zote.

Serikali imesema mafanikio hayo yametokana na juhudi za kuboresha mazingira ya biashara, kuvutia uwekezaji na kuimarisha shughuli za uzalishaji katika sekta mbalimbali za uchumi.

Kwa ujumla, mwenendo huo unaonyesha mwanga mpya katika soko la ajira nchini, huku matarajio yakiwa ni kuendelea kupungua kwa ukosefu wa ajira na kuongezeka kwa fursa zaidi kwa wananchi katika miaka ijayo.



Na mwandishi wetu, Zanzibar.

Katika  kuunga mkono juhudi za serikali ya awamu ya sita  la kukuza uchumi kwa wananchi wake  Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya imeamua mpango  kabambe ya kuhakikisha inaboresha soko lake la bidhaa pamoja na huduma mbalimbali lililopo katika Mji wa Mbalizi Tarafani ili kuchochea zaidi shughuli za kiuchumi na kuongeza hali ya ukusanyaji wa mapato kwa ajili ya kuharakisha   kwa  kuleta mabadiliko chanya ya kimaendeleo.

Mpango huo umekuja kufuatia ziara ya baraza la madiwani pamoja na jopo la wataalam kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, waliozuru visiwani Zanzibar, kuanzia tarehe 01 hadi 04 Juni 2026, kwa ajili ya mafunzo mbalimbali kuhusu mifumo ya uongozi katika sekta ya uchumi na kijamii kwa ajili ya kuleta maendeleo kwa wananchi kupitia fursa zinazowazunguka katika maeneo yao husika ya kiutawala.

Ziara hiyo ya mafunzo ilifanyika katika Baraza la Manispaa ya Magharibi B, inayoongozwa na Mkurugenzi Mtendaji, Bi. Sabra Issa Machano, ambapo ugeni wa baraza la madiwani na wataalam wanaounda menejimenti ya Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, walipata fursa ya kutembelea masoko makubwa mawili: Soko la Mwanakwerekwe na Soko la Jumbi.

Soko la Mwanakwerekwe ni soko lilijengwa baada ya kushirikisha wadau pamoja na uwezeshaji kupitia mkopo kutoka sekta binafsi kisha baadae serikali kuu kutoa fedha kwa ajili ya kumaridhia mradi huo.

Soko hilo linabeba wafanyabiashara takribani 5,224 tofauti na awali kabla ya kuboreshwa, ambapo lilikuwa linabeba wafanyabiashara 3,000 pekee. Uboreshaji huo umevutia karibu asilimia 50 ya wafanyabiashara wapya.

“Soko hili linafanya kazi saa 24 na linahudumia takribani watu 50,000 kwa siku. Ujenzi wake umezingatia kila aina ya watu kulingana na mahitaji yao. Hapa kuna maduka 187, vibanda 1,344, meza 152, bucha 18, maghala 12, vibanda vya kuegesha kwa biashara maarufu kama vigoli 56,” ameeleza Mkurugenzi Mtendaji wa Baraza la Manispaa ya Magharibi B.

Mfumo huo umewavutia zaidi madiwani pamoja na timu ya wataalam wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, waliokuwa katika ziara hiyo na kuweka azimio la kutaka kuboresha soko la Mbalizi, ambalo limekuwa kitovu kikubwa cha kibiashara katika Halmashauri. Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, Bi. Erica E. Yegella amesema Halmashauri inahitaji kuwa na soko la kisasa kama Mwanakwerekwe na Jumbi kwa ajili ya ustawi wa uchumi wa Halmashauri na wananchi wake.

Ameeleza kwamba Halmashauri inakusanya mapato ya ndani takribani shilingi bilioni nane (8) kwa mwaka, lakini ipo fursa ya kuboresha soko la Mbalizi hata kwa kupitia ubia na wadau wa maendeleo kutoka sekta binafsi ikiwemo taasisi za kifedha kama vile benki kwa ajili ya kuboresha soko hili linalobeba kiwango kikubwa cha wajasiriamali wakiwemo vijana wa kike na kiume sambamba na wanawake.

“Ziara yetu Zanzibar imekuwa na manufaa makubwa. Sote kama menejimenti na baraza letu la madiwani tumejionea kwa macho. Ipo fursa ya kuongeza mapato kupitia soko letu. Kinachotakiwa ni kuboresha miundombinu ya soko letu. Tuko tayari kuingia ubia na mdau yoyote ambaye anaweza kushirikiana nasi katika kuboresha sehemu hii kwa ajili ya kutengeneza mazingira rafiki ya biashara kwa wajasiriamali wetu.” Amesema Mkurugenzi Mtendaji Bi. Erica E. Yegella.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, Mhe. Aidda C. Haule, amesema Mji wa Mbalizi unakua kwa kasi kutokana na muingiliano mkubwa wa watu kupitia biashara mbalimbali. Amesema ujenzi wa masoko ya kisasa kama ilivyo kwa Zanzibar itasaidia pia kuhakikisha suala la mipango miji linazingatiwa kikamilifu pasina changamoto tofauti na ilivyo sasa, ambapo wafanyabiashara wametapakaa mpaka barabarani hali inayoleta usumbufu kwa watembea kwa miguu na watu wanaoendesha vyombo vya moto.

“Ziara hii imekuwa na tija kwetu kama Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya imetuonesha namna ambavyo tunaweza kushirikiana na wadau kuboresha masoko yetu, ambayo ni vituo muhimu kibiashara. Lakini pia tunaweza kuweka mazingira rafiki kwa wafanyabiashara pamoja na watoto wao kwa kujenga hata miundombinu ya kulelea watoto ndani ya soko letu kama ambavyo tumeona katika masoko ya hapa Zanzibar.” amesema Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya.

Halmashauri Wilaya ya Mbeya imemaliza ziara yake ya siku nne ambapo imewea kutembelea maeneo mbali mbali yaliyopo Visiwani Zanzibra ikiwemo eneo la unguja ambapo madiwani, wataalamu pamoja na Mkurugenzi wameweza kujifunza mambo mbali mbali  ambayo yataweza kuwa ni moja ya mkombozi mkubwa  katika utekelezaji wa majukumu yao ikiwemo suala la utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwa wananchi.





Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema Serikali itaendelea kushirikiana na taasisi na wadau mbalimbali wa sekta ya afya ili kuimarisha utoaji wa huduma bora za matibabu kwa wananchi.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, tarehe 11 Juni 2026, Ikulu Zanzibar, alipokutana na ujumbe wa Taasisi ya Humaniti ukiongozwa na Mtendaji Mkuu wake, Bw. Firaaz Azeez, pamoja na Mwanzilishi wa Doris Mollel Foundation, Bi.  Doris Mollel.

Amesema Serikali inathamini mchango wa Taasisi ya Humaniti katika kuimarisha sekta ya afya kupitia uwekezaji katika rasilimali watu, miundombinu na vifaa tiba, huku akisisitiza umuhimu wa kuimarisha mifumo endelevu ya afya badala ya kutegemea programu za muda mfupi.

Aidha, Rais Dkt. Mwinyi ameishukuru Taasisi ya Doris Mollel Foundation kwa juhudi zake za kusaidia huduma za afya kwa watoto wachanga na watoto wanaozaliwa kabla ya wakati, hatua inayochangia kuokoa maisha ya watoto hao.

Katika hatua nyingine, Taasisi ya Humaniti imemkabidhi Rais Dkt. Mwinyi hundi ya shilingi milioni 503 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba vya uchunguzi na matibabu ya magonjwa ya moyo kwa watoto.

Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa Humaniti, Bw. Firaaz Azeez, amepongeza maendeleo makubwa ya sekta ya afya Zanzibar baada ya kutembelea Hospitali za Lumumba, Chumbuni na Magomeni.
















Na Janeth Raphael MichuziTv Bungeni


Serikali ya Tanzania imetangaza vipaumbele vikuu vya Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa mwaka wa fedha 2026/27, ambao unalenga kuimarisha uchumi, kuboresha maisha ya wananchi na kuongeza ushindani wa taifa katika masoko ya kikanda na kimataifa.

Mpango huo umeelezwa kuwa dira muhimu ya maendeleo inayojikita katika maeneo matano makuu ya kimkakati. Kipaumbele cha kwanza ni kuimarisha utawala bora, amani, usalama na utulivu nchini, vikiwa ni msingi muhimu unaowezesha shughuli za kiuchumi na kijamii kukua kwa kasi na ufanisi.

Pia, serikali inalenga kujenga uchumi imara, jumuishi na shindani kupitia mageuzi katika sekta tisa muhimu ambazo zinatarajiwa kuwa kichocheo kikubwa cha ukuaji wa uchumi. Sekta hizo zitachangia kuongeza uzalishaji, kuvutia uwekezaji na kuimarisha ajira kwa wananchi.

Katika hatua nyingine, mpango huo umeweka msisitizo katika kuendeleza maendeleo ya watu kwa kuboresha huduma za kijamii ikiwemo afya, elimu na mafunzo ya stadi, ili kuongeza uwezo wa rasilimali watu na kuleta tija zaidi katika uchumi wa taifa.

Aidha, serikali imeelekeza nguvu katika kulinda mazingira na kuimarisha ustahimilivu dhidi ya mabadiliko ya tabianchi, sambamba na kukabiliana na majanga ya asili na yasiyo ya asili ambayo yamekuwa yakisababisha athari kwa maisha ya wananchi na uchumi kwa ujumla.

Kipaumbele kingine ni kuimarisha vichocheo vya maendeleo, hususan mifumo ya uwekezaji, matumizi ya teknolojia ya kisasa na ushirikiano kati ya sekta ya umma na binafsi, hatua inayotarajiwa kuongeza ufanisi na kasi ya maendeleo ya taifa.

Katika upande wa malengo ya uchumi jumla, mpango huo umeweka shabaha ya kukuza Pato Halisi la Taifa kufikia asilimia 6.3 mwaka 2026, kutoka asilimia 5.9 mwaka 2025. Aidha, mfumuko wa bei unatarajiwa kubaki katika wigo wa asilimia 3.0 hadi 5.0 ili kulinda uwezo wa wananchi kumudu gharama za maisha.

Serikali pia inalenga kuongeza mapato ya ndani kufikia asilimia 17.1 ya Pato la Taifa pamoja na mapato ya kodi kufikia asilimia 13.7 ya Pato la Taifa. Vilevile, nakisi ya bajeti inatarajiwa kubaki chini ya asilimia 3 ya Pato la Taifa, huku akiba ya fedha za kigeni ikidumishwa kwa kiwango kinachoweza kugharamia uagizaji wa bidhaa na huduma kwa angalau miezi minne.

Katika sekta ya ajira, mpango huo unalenga kuongeza fursa za ajira hadi kufikia milioni 1.7 ifikapo mwaka 2026, kutoka ajira 981,000 zilizozalishwa mwaka 2024, hatua inayotarajiwa kupunguza changamoto ya ukosefu wa ajira nchini.

Kwa upande wa utekelezaji, serikali imesisitiza kuwa mafanikio ya mpango huo yatategemea misingi muhimu ikiwemo kudumishwa kwa amani na utulivu, kuimarishwa kwa utawala bora na uwajibikaji pamoja na matumizi bora ya rasilimali za umma.

Vilevile, maendeleo ya miundombinu kama nishati, barabara, reli na bandari yamepewa kipaumbele ili kuiwezesha Tanzania kuwa kitovu cha biashara na usafirishaji katika ukanda wa Afrika Mashariki, Kati na Kusini.

Serikali pia imesisitiza umuhimu wa matumizi ya teknolojia na ubunifu wa kidijitali katika sekta mbalimbali, pamoja na mageuzi ya kitaasisi yanayoongozwa na falsafa ya 4Rs ili kuongeza ufanisi wa taasisi za umma.

Aidha, ushirikiano kati ya sekta ya umma na binafsi pamoja na fursa za kikanda kupitia Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na SADC umetajwa kuwa nguzo muhimu katika kuimarisha uwekezaji na biashara.

Akizungumzia mpango huo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo, amesema ni nyenzo muhimu ya kuhakikisha rasilimali za taifa zinatumika kwa ufanisi na kuleta matokeo yanayopimika katika kuharakisha maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

Kwa ujumla, Mpango wa Maendeleo wa 2026/27 unatarajiwa kuweka msingi imara wa kukuza uchumi jumuishi, kuongeza ajira na kuiweka Tanzania katika nafasi bora zaidi kuelekea uchumi wa kati wenye ushindani na ustahimilivu wa muda mrefu.


Na Ashura Mohamed, ARUSHA.

Naibu Mkuu wa Chuo, Upande wa Taaluma, Utafiti na Ushauri wa Kitaaluma kutoka Chuo cha Uhasibu Arusha IAA, Dkt. Grace Temba, ameweka jiwe la msingi kwa ajili ya maandalizi ya kongamano la kimataifa la utalii linalotarajiwa kufanyika tarehe 25 Septemba, 2026 mkoani Arusha.

Tukio hilo la kongamano ni muhimu kwa taasisi hiyo na maalum kwa wadau wa utalii kutoka maeneo mbali mbali duniani likilenga wadau wa sekta ya utalii kwa dhima kubwa ya kuhamasisha utalii wa ndani ili kuendelea kuhamasisha idadi ya watalii kuongezeka.

Akizungumza mara baada ya uzinduzi huo Dkt. Grace amesema kuwa lengo hasa ni kuhakikisha wadau mbali mbali wanashiriki na kufanya kongamano hilo kujumlisha watunga sera, wadau wa utalii kutoka ndani na nje ya nchi kujiandaa na kushiriki kwa ufanisi zaidi.

“Siku ya kongamano tunawaweka pamoja wadau mbali mbali tunatoa taarifa mbali mbali za utafiti zilizofanywa na wadau mbali mbali waliopo katika sekta ya utalii lakini pia Chuo cha Uhasibu Arusha, watunga sera wa taasisi na mlaji ili kuja na suluhisho na maboresho makubwa katika sekta ya utalii kwa lengo la kunufaisha pande zote,” alisema Dkt. Grace.

Aidha amesema kuwa kongamano hilo la nne linatarajiwa kuendelea kukuza na kutangaza nchi kimataifa kwa kuja na mawasilisho ambayo yatalenga wadau na watoa huduma kuendelea kujikuza kimasoko, miundombinu, na kuifanya sekta hiyo kuwa bobezi na kuchangia pato la taifa.

Nae Kaimu Mkuu wa Kitivo cha Biashara na Sayansi ya Jamii kutoka Chuo cha Uhasibu Arusha IAA, Bi. Lorna Boniface Mwijarubi, amesema kuwa chuo hicho kinatarajia kushirikiana na taasisi mbali mbali na wadau wa utalii katika kuonyesha tafiti na bunifu ambazo zitaisaidia sekta ya utalii kuwa bora zaidi na kuendelea kuliingizia taifa kipato.

Amesema kuwa mafanikio yaliyopatikana kutokana na makongamano yaliyopita ni makubwa kwa kuwa yamekijengea chuo mashirikiano na wadau ambayo huwezesha wanafunzi wa kozi ya utalii na ukarimu kupata fursa ya kujifunza kwa vitendo katika maeneo mbali mbali nchini na kusaidia kupata ajira pamoja na taifa kupata mapato kupitia sekta hiyo.

Chuo cha Uhasibu Arusha IAA kimeendelea kuwa maarufu katika sekta mbali mbali kwa kutoa elimu bora yenye ushindani sokoni huku katika sekta ya utalii inatajwa kuwa ndio chuo pekee kinachotoa kozi ya utalii na ukarimu nchini ambayo inatajwa kuwa na mchango mkubwa katika kutangaza nchi na kuendelea kuifanya sekta hiyo kuwa bora zaidi nchini.

Kaimu Mkuu  wa  chuo Upande wa Taaluma,Utafiti na   Ushauri wa kitaaluma kutoka cha Uhasibu Arusha(IAA), Dkt.Grace Temba Akiwa katika hafla hiyo iliyofanyika chuoni hapo.
Meneja Masoko na Ushirikiano na Mashirika kutoka hoteli ya Mount Meru Arusha bi.Lucy Foya akiwa katika hafla hiyo iliyofanyika chuo Cha Uhasibu Arusha
Wadau Mbali Mbali wakiwa katika picha ya Pamoja chuoni hapo


Na: Farida Mangube

Ufugaji wa ng’ombe wa maziwa katika Kata ya Igima, Wilaya ya Wanging’ombe mkoani Njombe, umeendelea kuwa chanzo kikuu cha mabadiliko ya kiuchumi kwa wananchi, baada ya uzalishaji kuongezeka na ubora wa maziwa kuboreka kutokana na elimu na utafiti unaotolewa na wataalamu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA).

Afisa Mifugo wa Kata ya Igima, SHAZI MOSES OKALA, amesema kata hiyo ina zaidi ya wafugaji 300 wa ng’ombe wa maziwa wenye zaidi ya ng’ombe 700, ambapo kwa sasa huzalisha zaidi ya lita 2,500 za maziwa kwa siku. Amesema maziwa hayo hukusanywa kupitia vituo vya ukusanyaji kabla ya kupelekwa kwenye kituo cha kupoozea na baadaye kusafirishwa kwa ajili ya usindikaji.

Yokara amesema kabla ya kuanza kwa elimu na utafiti wa wataalamu wa SUA kupitia Mradi wa NANOCOM, wafugaji walikuwa wakikabiliwa na changamoto ya magonjwa ya mifugo hususan homa ya kiwele (mastitis), hali iliyosababisha maziwa mengi kuchachuka na kupoteza ubora wake. Hata hivyo, ameeleza kuwa hali hiyo imepungua kwa kiasi kikubwa baada ya wafugaji kupewa elimu ya usafi wa mabanda na mbinu bora za ufugaji.

Ameongeza kuwa elimu hiyo imechangia si tu kuboresha afya ya mifugo, bali pia kuongeza uzalishaji wa maziwa na kipato cha wafugaji, ambapo sasa maziwa mengi yanakidhi viwango vya soko tofauti na ilivyokuwa awali.

Katika hatua nyingine, mfugaji na kiongozi wa kikundi cha Beach Group, Bi. Liones Richard, ameeleza jinsi ufugaji ulivyobadilisha maisha yake tangu alipoanza mwaka 2007 akiwa na ng’ombe mmoja pekee, ambapo kwa sasa anamiliki ng’ombe wanne wanaozalisha zaidi ya lita 20 za maziwa kwa kila ng’ombe kwa siku.

Bi. Liones amesema mafanikio hayo yametokana na matumizi ya mbinu bora za ufugaji na ushauri wa kitaalamu anaoupata, ambao umemsaidia kuboresha lishe ya mifugo, afya ya ng’ombe na usafi wa mabanda, hivyo kuongeza uzalishaji kwa kiwango kikubwa.

Amehitimisha kwa kusema kuwa mafanikio hayo yamemuwezesha kujenga nyumba bora na kuwapatia watoto wake elimu, huku akiwahamasisha wanawake, vijana na wafugaji wengine kuona ufugaji wa ng'ombe wa maziwa kama fursa muhimu ya kiuchumi inayoweza kubadilisha maisha endapo itafanyika kwa weledi na maarifa sahihi.





Historia ya Tanzania katika harakati za kupigania uhuru, kuundwa kwa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar pamoja na mchango wake katika ukombozi wa Afrika ni miongoni mwa vivutio vitakavyopewa nafasi ya kipekee katika Maonesho ya Kiswahili yatakayofanyika jijini Paris, Ufaransa, sambamba na Kongamano la Pili la Kiswahili la Kimataifa.

Maonesho hayo yatakayofanyika katika viunga vya Makao Makuu ya UNESCO kuanzia Julai 4 hadi 7, 2026, yanatarajiwa kuwakutanisha washiriki kutoka mataifa mbalimbali duniani kwa lengo la kuendeleza matumizi ya Kiswahili na kuonesha mchango wake katika amani, mshikamano na diplomasia ya uchumi duniani.

Kwa mujibu wa mwongozo wa kongamano hilo, sehemu maalum ya maonesho itajikita katika kuonesha historia ya uhuru wa Tanzania, hatua za kuundwa kwa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar pamoja na nafasi ya Tanzania katika kuunga mkono harakati za ukombozi wa mataifa mbalimbali ya Afrika yaliyokuwa chini ya ukoloni.

Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) ni miongoni mwa taasisi za Serikali chini ya Wizara ya Habari, Utamaduni Sanaa na Michezo, zitakazotuma uwakilishi wa kushiriki kwa mara ya kwanza katika kongamano hilo.

Akizungumza jijini Dar es Salaam tarehe 11 Juni, 2026 kuhusu Kongamano hilo, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB), Wakili Patrick Kipangula, amesema lengo la kutuma uwakilishi wa Taasisi ni kujifunza uzoefu wa kimataifa, kuimarisha ushirikiano na wadau wa lugha na vyombo vya habari kutoka mataifa mbalimbali pamoja na kuendeleza mchango wa Tanzania katika kukuza Kiswahili.

Washiriki watapata fursa ya kujifunza mchango wa Tanzania katika kujenga mshikamano wa Afrika na kuimarisha ushirikiano wa kimataifa kupitia diplomasia, huku vielelezo mbalimbali vikionesha nafasi ya taifa hilo kama kitovu cha harakati za ukombozi wa Bara la Afrika.

Katika kuongeza mvuto wa maonesho hayo, nukuu za viongozi mashuhuri wa Tanzania, akiwemo Baba wa Taifa Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, zitaoneshwa kupitia skrini kubwa kwa lengo la kuhamasisha maadili ya uongozi, amani, umoja na maendeleo.

Aidha, maonesho hayo yataangazia mchango wa lugha ya Kiswahili katika diplomasia ya Afrika na nafasi yake katika kuimarisha utangamano wa watu wa mataifa mbalimbali, sambamba na juhudi zinazoendelea za kukitangaza Kiswahili kama lugha ya kimataifa inayobeba historia, utamaduni na utambulisho wa Waafrika.

Kongamano la Pili la Kiswahili la Kimataifa linaandaliwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushirikiana na UNESCO chini ya kaulimbiu ya “Kiswahili kwa Amani, Mshikamano na Diplomasia ya Uchumi Duniani,” likiwa sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Kiswahili Duniani inayoadhimishwa kila mwaka Julai 7.

Na Janeth Raphael MichuziTv - Bungeni Dodoma 

SERIKALI imesema Kamati za Watu Wenye Ulemavu zilizoanzishwa katika ngazi za Mkoa, Wilaya, Vijiji na Mitaa zinaendelea kutekeleza majukumu yake kwa mujibu wa Sheria ya Watu Wenye Ulemavu Na. 9 ya Mwaka 2010, huku utekelezaji wa majukumu hayo ukifikia asilimia 52.

Kauli hiyo imetolewa bungeni na Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI), Dkt Festo Ndugange alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Stella Ikupa Alex, aliyetaka kufahamu kama kamati hizo zinafanya kazi katika maeneo mbalimbali nchini.

Dkt Ndugange amesema sheria imezipa kamati hizo jukumu la kufuatilia upatikanaji wa huduma muhimu kwa watu wenye ulemavu, ikiwemo afya, elimu, ajira, ulinzi wa jamii pamoja na miundombinu jumuishi.

Aidha, kamati hizo zina wajibu wa kushauri Sekretarieti za Mikoa na Halmashauri kuhusu masuala yanayohusu watu wenye ulemavu, kufuatilia utekelezaji wa mipango na bajeti zinazowahusu, pamoja na kupokea na kujadili changamoto zinazowakabili na kupendekeza ufumbuzi wake.

Katika hatua nyingine, Dkt  Ndugange amesema kupitia kamati hizo, jumla ya watu wenye ulemavu 328,733 wametambuliwa nchini kote. Kati yao, wanaume ni 162,464 huku wanawake wakiwa 166,269.

Ameeleza kuwa utambuzi à sasa àhuo umeiwezesha Serikali kupata takwimu sahihi zinazotumika katika upangaji, utekelezaji na ufuatiliaji wa huduma mbalimbali za kijamii kwa watu wenye ulemavu.

Serikali imeahidi kuendelea kusimamia na kuhakikisha kamati hizo zinafanya kazi kwa ufanisi na kwa kuzingatia matakwa ya sheria ili kuimarisha ustawi na ushiriki wa watu wenye ulemavu katika maendeleo ya taifa.


Wananchi wa Jimbo la Kilindi wamepokea kwa furaha taarifa ya Serikali kutoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa shule mpya ya sekondari katika Kata ya Msanja, Kijiji cha Muungano Jimbo la Kilindi, Hatua hiyo inalenga kuongeza fursa za elimu kwa vijana pamoja na kuboresha mazingira ya kujifunzia katika eneo hilo.

Mradi huo unatarajiwa kuanza kutekelezwa mara moja na utasaidia kupunguza changamoto ya wanafunzi kusafiri umbali mrefu kufuata huduma za elimu ya sekondari, hali itakayowezesha upatikanaji wa elimu kwa urahisi zaidi kwa wakazi wa Kata ya Msanja na maeneo jirani.

Akizungumza kuhusu maendeleo hayo, Juni 11, 2026, Mbunge wa Jimbo la Kilindi, Mhe. Salehe Mbwana Mhando, ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kuwekeza katika sekta ya elimu na kutekeleza miradi ya maendeleo inayogusa maisha ya wananchi moja kwa moja.

Wananchi wa Kata ya Msanja na Jimbo la Kilindi kwa ujumla wameeleza shukrani zao kwa Serikali kwa kuendelea kuwaletea miradi ya maendeleo yenye manufaa kwa jamii, aidha wameahidi kutoa ushirikiano unaohitajika ili kuhakikisha mradi huo unakamilika kwa wakati na kwa viwango vinavyostahili.



Waziri wa Mambo ya Nje na Masuala ya Ulaya wa Jamhuri ya Slovakia, Mhe. Juraj Blanár, amewasili nchini kwa ziara ya kikazi kuanzia Juni 10 hadi 11, 2026, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia na ushirikiano kati ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Jamhuri ya Slovakia.

Katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) jijini Dar es Salaam Mhe. Juraj Blanár alilakiwa na Naibu Waziri Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayeshughulikia masuala ya Afrika Mashariki Mhe. James Milya (Mb).

Akiwa nchini, Mhe. Blanár atashiriki katika mazungumzo ya pande mbili na mwenyeji wake, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Dkt. Mahmoud Thabit Kombo (Mb.) yatakayofanyika Juni 11 2026.

Ziara hii inalenga kuimarisha ushirikiano katika sekta mbalimbali ikiwemo utalii, elimu, programu za ufadhili wa masomo, usalama wa mtandao, biashara na uwekezaji.

Baada ya mazungumzo na mwenyeji wake watazungumza na waandishi wa habari na baadaye watashiriki katika hafla ya uzinduzi wa Ubalozi wa Jamhuri ya Slovakia jijini Dar es Salaam. Ubalozi huo ulifunguliwa mwezi Novemba 2025 na unaashiria dhamira ya pamoja ya Tanzania na Slovakia ya kuimarisha zaidi uhusiano wa kidiplomasia pamoja na kupanua maeneo ya ushirikiano wa maendeleo na uchumi.

Waziri Blanár ambaye ameambatana na wafanyabiashara wapatao 50 atashiriki katika Kongamano la Biashara la Tanzania Slovakia litakalokutanisha wafanyabiashara na wawakilishi wa sekta binafsi kutoka nchi zote mbili. 

Kongamano hilo linatarajiwa kujadili fursa za biashara na uwekezaji, kukuza uhamishaji wa teknolojia na kuimarisha ushirikiano katika sekta za kimkakati zikiwemo nishati jadidifu, uchakataji wa mazao ya kilimo na ubunifu wa kidijitali.

















-Ahimiza kuwekeza kwenye miundombinu inayochochea vyanzo vya uwekezaji.

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali itaendelea kuondoa vikwazo na kuimarisha ushirikiano na sekta binafsi ili kuboresha mazingira ya uwekezaji nchini.

Ameyasema hayo leo (Jumatano, Juni 10, 2026), wakati akizindua ghala la forodha la kampuni ya Ciwaye Trading Co. Ltd Wilayani Chamwino mkoani Dodoma.

“Kama tunavyoheshimu sekta ya umma, tunatakiwa kuheshimu sekta binafsi kwa uzito ule ule, kama mataifa mengine yaliyoendelea, uchumi wa mataifa hayo nguzo yake ni sekta binafsi.”

Dkt. Mwigulu aliongeza kwa kusema “Kwa kuheshimu hilo, nimeona nije kuzindua mradi huu, kama ambavyo nimepita kwenye ziara kuzindua miradi ya Serikali, ndiyo maana nimeona na hapa nije mwenyewe.”

Aidha, ameeleza kuwa mradi huo una umuhimu mkubwa katika maendeleo ya nchi, hivyo hauna budi kulelewa.

“Ukubwa wa jambo hili haupimwi kwa majengo, bali kwa uthubutu na matokeo yanayoakisi Dira yetu ya maendeleo na maono ya Rais wetu ya kuhakikisha mradi kama huu unatoa matokeo yaliyokusudiwa.” Amesisitiza Waziri Mkuu Mwigulu.

Waziri Mkuu ameongeza kuwa mradi huo unatazamwa na Serikali kama mradi wa kielelezo wa kutekeleza Dira 2050 na ndiyo maana Serikali imekuwa ikiboresha mazingira ya uwekezaji nchini, ikiwemo maboresho ya sheria za uwekezaji.

“Zimebadilishwa Sheria za uwekezaji ili kuhakikisha wazawa wananufaika na kuushika uchumi, zamani vivutio vya uwekezaji viliwanufaisha wageni, lakini sasa wazawa wanapata vivutio hivyo,” ameeleza Waziri Mkuu.

Ameongeza kuwa: “Mfano katika sekta ya uzalishaji, zamani miradi yote mikubwa ilikuwa inatekelezwa na wageni, lakini mabadiliko hayo ya sheria yamewezesha wazawa kutekeleza miradi mikubwa, na sasa wanaweza kuajiri wageni katika utekelezaji wa miradi hiyo.”

Waziri Mkuu Mwigulu amesema mkakati mwingine unaoenda sambamba na mabadiliko ya sheria, ni pamoja na kuondoa zaidi ya tozo 270 ili kuwapunguzia mzigo wafanyabiashara na walaji wa mwisho.

Akizungumzia utekelezaji wa mradi huo, Waziri Mkuu ameeleza kufurahishwa na hatua zilizofikiwa katika utekelezaji wake, kwani umetekelezwa ndani ya muda mfupi lakini viwango vya ubora vimezingatiwa.

Amesema uamuzi wa kuanzisha ghala hilo mkoani Dodoma ni wa kimkakati kwani Dodoma ipo katikati ya nchi, ikiunganisha maeneo mengine ya nchi na fursa zilizopo katika maeneo hayo, ambapo amewataka wafanyakazi wa mradi huo kuwa waaminifu ili mradi uwe na faida endelevu, kwao binafsi na jamii.

Pia Waziri Mkuu Mwigulu amewahimiza Wakuu wa Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kuhamasisha wawekezaji kuwekeza kwenye mikoa na maeneo yao kwa kuweka miundombinu inayochochea vyanzo vya mapato na kukua kwa uchumi.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu Mwigulu ameuagiza Wakala wa Barabara za Mijini na Vijini (TARURA) kukaa kwa haraka na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) na kufanya tathmini ya ujenzi wa barabara ya kiwango cha lami ya kilometa 25 kuanzia Chamwino kwenda kituo cha treni cha Igandu ili kusaidia ufanisi wa ghala lililojengwa kwani barabara hiyo itaunufaisha mradi huo.

Kwa upande wake Meneja Masoko wa ghala hilo, Leroy Nelson amesema mradi huo umegharimu zaidi ya shilingi bilioni tatu ambapo utekelezaji wake umekamilika kwa asilimia 100.







Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imeshiriki uzinduzi wa Ghala la Forodha la Kampuni ya Ciwaye lililopo Chamwino mkoani Dodoma, hatua inayolenga kuhamasisha ulipaji wa kodi kwa hiari na kuongeza fursa za uwekezaji wa kibiashara katika mkoa huo.

Akizungumza kwa niaba ya Kamishna Mkuu wa TRA katika hafla hiyo iliyozinduliwa na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, Naibu Kamishna wa Shughuli za Forodha, Wahabi Matengo, Juni 10, 2026,  amesema ghala hilo ni la kwanza la aina yake katika Mkoa wa Dodoma na lina mchango mkubwa katika kuwezesha biashara halali na kukuza uchumi.

Matengo amesema maghala ya forodha ni nyenzo muhimu inayotolewa kwa mujibu wa Sheria ya Forodha ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya mwaka 2004 iliyofanyiwa marejeo mwaka 2025 pamoja na Kanuni za Forodha za mwaka 2010.

Ameeleza kuwa ghala hilo limeanzishwa kwa ajili ya kuhifadhi magari madogo na makubwa, matrela pamoja na mitambo mbalimbali, huku bidhaa zote zikiwa chini ya usimamizi wa Idara ya Forodha na Ushuru wa Bidhaa hadi zitakapokamilisha taratibu za kiforodha na kulipiwa kodi stahiki.

Akifafanua faida za maghala ya forodha, Matengo amesema mfumo huo hurahisisha ulipaji wa kodi kwa kuwa wafanyabiashara wanaweza kuingiza bidhaa nchini na kuzihifadhi ghalani bila kulipa kodi mara moja, Kodi hulipwa pale bidhaa zinapotolewa kwa matumizi ya ndani ndani ya kipindi kisichozidi mwaka mmoja tangu kuhifadhiwa kwake.

Aidha, amesema maghala hayo yanakuza biashara ya kimataifa kwa kuruhusu bidhaa zilizohifadhiwa kuuzwa ndani na nje ya nchi, sambamba na kuongeza mtiririko wa fedha kwa wafanyabiashara kwani fedha ambazo zingetumika kulipia kodi mara moja hutumika kuimarisha mitaji ya biashara.

Faida nyingine alizozitaja ni pamoja na kuhakikisha upatikanaji wa bidhaa kwa wakati pamoja na kurahisisha matumizi ya misamaha ya kodi kwa wafanyabiashara wanaostahili kwa mujibu wa sheria.

Matengo ameihakikishia Kampuni ya Ciwaye ushirikiano wa karibu kutoka TRA pamoja na utoaji wa miongozo mbalimbali ili kuhakikisha shughuli zote za ghala hilo zinafanyika kwa kuzingatia sheria na kuchangia ukuaji wa mapato ya serikali pamoja na maendeleo ya uchumi wa Mkoa wa Dodoma na Taifa kwa ujumla.

Kwa upande wake, Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba amesema Serikali imeendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ya kuboresha mazingira ya biashara nchini, ikiwemo kupunguza tozo na kufanya marekebisho ya sheria kadhaa ili kuimarisha sekta ya uwekezaji na biashara.

Amesema Serikali inatarajia kuona utekelezaji wa baadhi ya mapendekezo yaliyotolewa na wadau kuanza kuleta matokeo yanayoakisi matarajio ya wananchi, huku lengo kuu likiwa ni kuongeza idadi ya wawekezaji wazawa watakaoshiriki kikamilifu katika kukuza uchumi wa nchi.







Top News