Awali akizungumza Mkuu wa Chuo na Mtendaji Mkuu Dkt. Ernest Mabonesho, amesema kongamano hilo limeandaliwa kama jukwaa la kuwakutanisha wadau mbalimbali kwa lengo la kujadiliana na kubadilishana uzoefu kuhusu namna bora ya kuimarisha utendaji wa taasisi za umma katika mazingira yanayobadilika kwa kasi.
Awali akizungumza Mkuu wa Chuo na Mtendaji Mkuu Dkt. Ernest Mabonesho, amesema kongamano hilo limeandaliwa kama jukwaa la kuwakutanisha wadau mbalimbali kwa lengo la kujadiliana na kubadilishana uzoefu kuhusu namna bora ya kuimarisha utendaji wa taasisi za umma katika mazingira yanayobadilika kwa kasi. Wananchi waliotembelea banda la Wakala wa Vipimo (WMA) katika Maonesho ya Kitaifa ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali Park, Dodoma, wameeleza kufurahishwa na elimu wanayoipata kuhusu matumizi sahihi ya vipimo na kuahidi kuwa mabalozi wa kuelimisha jamii kuhusu umuhimu wa kuhakiki vipimo katika shughuli za kila siku.
Siku ya tatu ya maonesho hayo yaliyofunguliwa Juni 16 na yanayotarajiwa kuhitimishwa Juni 23, 2026, banda la WMA limeendelea kuvutia idadi kubwa ya wananchi wanaotaka kujifunza namna Serikali inavyohakikisha vipimo vinavyotumika katika biashara na huduma mbalimbali vinakuwa sahihi na vya kuaminika.
Mmoja wa wananchi hao, Bw. Bilson Vedastus, alisema elimu aliyopata imemsaidia kuelewa mambo muhimu ya kuzingatia anaponunua mafuta, gesi ya kupikia na bidhaa nyingine zinazopimwa.
“Awali sikuwa naelewa mambo haya kwa kina, lakini sasa najua ninachopaswa kuangalia ninapojaza mafuta, kununua sukari au gesi ya kupikia,” alisema.
Kwa upande wake, Bi. Asha Siyaya alisema elimu hiyo imewapa uwezo wa kutambua udanganyifu unaoweza kufanywa kupitia vipimo visivyo sahihi na kuahidi kutoa taarifa pale watakapobaini ukiukwaji.
“Tumeona jinsi pampu za mafuta, mizani na vifaa vingine vinavyohakikiwa ili kuhakikisha vinapima kwa usahihi. Hatuwezi kukaa kimya tukiona mteja anadhulumiwa. Tutawaeleza wengine na kuripoti udanganyifu popote tutakapouona,” alisema.
Wataalamu wa WMA, Albogast Kajungu, Mbwana Amani na Said Ibrahim, waliwaeleza wananchi kuwa huduma za uhakiki wa vipimo zinagusa sekta nyingi zinazohusiana moja kwa moja na maisha ya kila siku ya wananchi.
Walifafanua kuwa pampu za mafuta huhakikiwa na kuwekewa alama za uthibitisho, huku mizani inayotumika sokoni na madukani kupimia bidhaa mbalimbali ikikaguliwa mara kwa mara ili kuhakikisha watumiaji wanapata kiwango stahiki cha bidhaa wanazonunua.
Aidha, mita za maji na umeme zinazotumika majumbani na katika biashara huhakikiwa ili kuhakikisha wateja wanalipia matumizi halisi, huku mitungi ya gesi ya kupikia, bidhaa zilizofungashwa pamoja na mizani za kupimia uzito wa magari barabarani nazo zikiendelea kufanyiwa ukaguzi wa mara kwa mara.
Akizungumza na waandishi wa habari, Meneja Mawasiliano wa Wakala wa Vipimo, Bi. Veronica Simba, alisema lengo la WMA ni kuhakikisha kila mwananchi anapata thamani halisi ya fedha anayolipia bidhaa na huduma mbalimbali.
Alitoa wito kwa wananchi kuendelea kutembelea banda la WMA katika maonesho hayo ili kupata elimu zaidi kuhusu haki zao na umuhimu wa matumizi ya vipimo sahihi katika shughuli za kijamii na kiuchumi.



Na Mwandishi Wetu
KATIBU Mkuu Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji anayeshugulikia Uwekezaji, Dkt. Fred Msemwa amesema kufanikiwa kwa utekelezaji wa Dira 2050 kutategemea sana Uwezo,ufanisi na ubunifu wa sekta ya umma.
Amesema sekta ya umma ina jukumu la kuzidi kuboresha utendaji wake kutoka shughuli za utawala wa kawaida kwenda katika utendaji wenye matokeo, utendaji unaowalenga wananchi na unaojali matokeo.
Dk.Msemwa hayo alipokuwa akizungumza njia ya mtandao wakati wa Kongamano la Pili la Utumishi wa Umma Tanzania 2026 lililofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNCC) jijini Dar es Salaam,
Akieleza zaidi wakati wa kongamano hilo amefafanua pia kuna mambo matano zaidi ya kuweza kuyafanyiwa kazi zaidi ili kuimarisha utekelezaji wa Dira 2050.
Ametaja jambo la kwanza ni kuchochea utamaduni wa uvumbuzi ambapo amesema sekta ya umma lazima iweke mazingira ya kuweza mawazo mapya na majawabu mapya kwa matatizo ya wananchi. Ni muhimu kuongeza ushirikiano na vyuo, taasisi za utafiti pamoja na sekta binafsi ili kuchochea upatikanaji wa mawazo mapya.
Pia jambo la pili ni kutoa huduma kwa kuwafikiria wananchi ambapo amefafanua mifumo ya utoaji huduma ni muhimu ilenge mahitaji ya wananchi na shughuli zao za kiuchumi. Hivyo sekta ya umma irahisishe taratibu na mifumo yake ili ifikike kiharisi.
“Lazima kuwa na huduma jumuishi na zinazofikika na kuwa na uwezo wa kupata mrejesho kutoka kwa wananchi.”
Wakati jambo la tatu ni kuimarisha ushirikiano na sekta binafsi ambapo amesema Ili kufikia malengo ya Dira2050 ambayo inaipa nafasi kubwa sekta binafsi katika kufanikisha malengo yetu ya kiuchumi.
“Sekta ya umma ni lazima iweke mazingira bora kwa ajili ya kukuza Ujasiriamali, uwekezaji na ujenzi wa miundombinu. Ushirikiano huu ni muhimu katika kuleta si tu umoja wa kitaifa lakini pia kuzalisha ajira, kuleta ufanisi katika uzalishaji na utoaji huduma.”
Jambo la nne ni kuimarisha utaratibu wa kisera na serikali ifikirie kama mtu mmoja.Serikali imepiga hatua kubwa katika kuweka mifumo bora ya utendaji na ufuatiliaji wa shughuli zake. Ni muhimu kwa serikali kuendelea kuimarisha mifumo hiyo ili kuleta ufanisi zaidi.
Wakati jambo la tano ni kubadili mtizamo ,ambapo amesema Dira 2050 ina malengo makubwa na ufikiaji wa malengo utahitaji kufanyika kwa mambo katika utaratibu usio wa kawaida.
“Ni muhimu kwa serikali kuendelea kufanya maboresho na kupunguza urasimu na kulenga katika kasi na ubora wa huduma. Kuhama kutoka katika mifumo inayodhibiti shughuli za sekta binafsi kwenda katika kuwezesha sekta binafsi, kuwa na mtizamo wa muda mrefu badala ya kufikiria malengo ya muda mfupi,”amesema Dk.Msemwa.
NA Mashaka Mhando, Iringa
SERIKALI imetenga kiasi cha Shilingi Bilioni 15 katika mwaka wa fedha 2026/2027 kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa Akademia ya Taifa ya Michezo iliyopo Chuo cha Maendeleo ya Michezo Malya.
Hatua hiyo ya kiserikali inalenga kuweka mfumo thabiti na wa kudumu wa kuibua, kulelea, na kukuza vipaji vinavyopatikana kupitia mashindano ya shule za msingi na sekondari (UMITASHUMTA na UMISSETA).
Hayo yamebainishwa jana, Juni 17, 2026, na Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Hamis Mwinjuma (MwanaFA), wakati akifunga rasmi mashindano ya UMITASHUMTA yaliyokuwa yakifanyika mkoani Iringa.
Mhe. Mwinjuma alieleza kuwa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan inaendelea kuwekeza kwa nguvu kubwa katika sekta ya michezo na sanaa, ikitambua mchango wake katika kuzalisha ajira, kujenga afya, na kuongeza ushindani wa Taifa kimataifa.
Malya Academy na Matunda ya Serengeti Boys
Akifafanua kuhusu matumizi ya Akademia hiyo ya Malya, Mhe. Mwinjuma alisema kituo hicho kitakuwa na uwezo mkubwa wa kupokea na kuendeleza vipaji vinavyogunduliwa kwenye mashindano ya shule, ili kuandaa kizazi cha dhahabu kitakachowakilisha Taifa.
Kuthibitisha ubora wa mashindano hayo, Naibu Waziri aliweka wazi matokeo chanya yaliyoonekana hivi karibuni kupitia Timu ya Taifa ya Vijana chini ya miaka 17 (Serengeti Boys).
"Mafanikio ya Serengeti Boys yameonyesha umuhimu wa kuendelea kuwekeza kwenye michezo ya shule. Wachezaji wasiopungua watano wa kikosi hicho, akiwemo golikipa namba moja, ni zao halisi lililotokana na mashindano ya UMITASHUMTA na UMISSETA," alibainisha Mhe. Mwinjuma.
Maandalizi ya FEASSSA Morogoro
Aidha, Mhe. Mwinjuma alihitimisha kwa kueleza kuwa mashindano yaliyofungwa Iringa ni msingi muhimu wa kuandaa wawakilishi wa Tanzania watakaoshiriki Mashindano ya Michezo ya Shule kwa Nchi za Afrika Mashariki (FEASSSA).
Mashindano hayo makubwa ya kikanda yanatarajiwa kufanyika mwezi Agosti mwaka huu mkoani Morogoro, ambapo Naibu Waziri amewataka wanamichezo wote waliochaguliwa kuunda timu ya Taifa kambi kufanya maandalizi kabambe ili kuitangaza vyema Tanzania na kubakiza makombe nyumbani.
Serikali imesema Tanzania bado haina mgonjwa wa Ebola na imeendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuimarisha ulinzi dhidi ya ugonjwa huo pamoja na kusaidia juhudi za kikanda za kudhibiti maambukizi.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma leo, Waziri wa Afya, Mohamed Mchengerwa, amesema Serikali imeweka mikakati madhubuti ya kuhakikisha nchi inabaki salama dhidi ya tishio la ugonjwa huo unaoendelea kuripotiwa katika baadhi ya nchi jirani.
Amesema miongoni mwa hatua zilizochukuliwa ni kuhakikisha upatikanaji wa kutosha wa vifaa kinga katika bohari za dawa, kusimika maabara mbili za ziada kwa ajili ya uchunguzi na upimaji wa wagonjwa wanaoshukiwa kuwa na Ebola, pamoja na kuimarisha mifumo ya ufuatiliaji na uchunguzi katika maeneo yote ya mipakani na vituo vya kutolea huduma za afya.
Aidha, zaidi ya watu 45,000 wamefikiwa na mafunzo kuhusu njia za kujikinga dhidi ya ugonjwa wa Ebola, hatua inayolenga kuongeza uelewa wa jamii na kuimarisha utayari wa taifa kukabiliana na mlipuko wowote utakaoweza kujitokeza.
Waziri Mchengerwa amesema Tanzania imeendelea kushiriki kikamilifu katika juhudi za kikanda za kupambana na Ebola, akisisitiza kuwa usalama wa afya wa nchi jirani ni sehemu muhimu ya usalama wa afya wa Tanzania.
Amesema kupitia uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, Tanzania imeendelea kutoa ushirikiano kwa nchi jirani zilizoathirika na ugonjwa huo, ambapo tayari vifaa tiba vyenye thamani ya zaidi ya Shilingi milioni 500 vimetolewa kusaidia Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo na Uganda katika kukabiliana na ugonjwa huo.
Pamoja na hatua hizo, Serikali imefafanua kuwa haijafunga mipaka yake, bali imeimarisha mifumo ya udhibiti, uchunguzi na ufuatiliaji katika maeneo yote ya kuingilia na kutoka nchini ili kuzuia kuingia kwa maambukizi.
Aidha, Waziri Mchengerwa amesisitiza kuwa mafanikio katika mapambano dhidi ya Ebola yanahitaji ushirikishwaji wa wadau wote, ikiwemo sekta binafsi, mashirika mbalimbali na wananchi kwa ujumla, kwani jukumu la kudhibiti ugonjwa huo haliwezi kubebwa na Serikali pekee.
WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amewataka watendaji wa Wizara ya Maji pamoja na Wakuu wa Mikoa wasimamie vizuri mitambo ya uchimbaji visima ili iweze kufanya kazi iliyokusudiwa.
Amesema Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan alinunua mitambo ya uchimbaji wa visima hivyo watendaji wachukue hatua na waache kufanya kazi kwa mazoea.
"Nielekeze Wakuu wa Mikoa yote pamoja na wizara, kusimamia ili mitambo ile iweze kufanya kazi iliyokusudiwa, ni kweli kuna baadhi ya maeneo ya tunaendelea endelea na ile tabia ya business as usual, sasa ili kufikia matokeo ya Dira 2050, ni lazima tufanye kazi business unusual, tuache kufanya kazi kwa kuchukulia vitu kimazoea mazoea", Ameelekeza Waziri Mkuu.
Dkt. Mwigulu ametoa maelekezo hayo leo (Alhamisi Juni 18, 2026) Bungeni jijini Dodoma katika kipindi cha Maswali kwa Waziri Mkuu wakati akijibu swali la Mbunge wa Kwimba, Cosmas Bullala.
Mbunge huyo alitaka kujua kauli ya Serikali kuhusu ufanisi wa mitambo hiyo, ambapo Mheshimiwa Dkt. Mwigulu amesema mitambo hiyo inaendelea kuchimba visima katika maeneo mbalimbali nchini. Ambapo kwa sasa unatekelezwa mpango wa uchimbaji visima 900.
Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu Mwigulu amesema Serikali inatarajia kuanza kuwalipa kifuta jasho askari waliojitolea katika vita dhidi ya Idd Amin wa Uganda mwaka 1978-79.
Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu ameeleza hayo wakati akijibu swali la Mbunge wa Njombe, Deodatus Mwanyika aliyetaka kujua ni lini Serikali itawalipa kifuta jasho askari hao, ambapo Waziri Mkuu Mwigulu amesema tayari Serikali imefanya mabadiliko ya Sheria ambapo sasa askari hao wanatambulika kisheria kutokana na hapo mwanzo kutotambuliwa.
“Mheshimiwa Spika, Sheria za zamani zilikuwa haziwatambui wapiganaji wale, hasa hasa wapiganaji waliopata mafunzo ya muda mfupi, hivi tunavyoongea, kupitia tangazo la Serikali la mwezi wa 6, mwaka 2025, kuhusu mabadiliko ya Sheria ya mafao ya veterani, sasa imeshawatambua wapiganaji hao”, Amesema Dkt. Mwigulu.
“Mheshimiwa Spika, wapiganaji hao wataanza kulipwa na watalipwa kwa kuwa sasa hakuna kikwazo cha kisheria ambacho kilikuwa kinawakwamisha, na kile cha uhakiki, kwani wapiganaji hao wameshahakikiwa”, Amesisitiza Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu.
Walimu walioko kazini pamoja na vijana ambao hawakufanikiwa kuendelea na elimu ya juu wametakiwa kutumia fursa zinazotolewa na vyuo vya elimu ya ujuzi vinavyotoa mafunzo kwa njia ya masafa ili kujiendeleza na kupata maarifa mapya yatakayowasaidia kukabiliana na mtaala mpya wa elimu.
Wito huo umetolewa wakati wa mahafali ya nne ya wahitimu wa DC Polytechnic Education Institute College kilichopo Halmashauri ya Bukoba mkoani Kagera, ambapo jumla ya wanafunzi 908 walihitimu katika ngazi za shahada na astashahada katika fani mbalimbali zikiwemo ualimu, utawala, uongozi, mawasiliano, teknolojia na ufundi.
Akizungumza katika Kongamano la Wahitimu (Convocation) la chuo hicho, Mkurugenzi wa Huduma za Jamii kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dkt. Elieth Lulu Niwagila, alisema Tanzania kwa muda mrefu imekuwa ikitekeleza mfumo wa elimu uliolenga zaidi utoaji wa maarifa ya darasani, lakini kwa sasa serikali imefanya maboresho makubwa ya mtaala ili kuzalisha wahitimu wenye umahiri, ubunifu na uwezo wa kutatua changamoto mbalimbali za jamii.
Alisema wataalamu wa elimu wamejiridhisha na mabadiliko hayo ya mtaala na kwamba walimu walioko kazini wanapaswa kujiendeleza ili kuendana na mahitaji ya mfumo mpya wa elimu.
“Niseme kwamba sisi kama wataalamu wa masuala ya elimu tumevutiwa sana na mabadiliko haya. Dunia imebadilika sana na kinachohitajika sasa ni ujuzi. Serikali imeamua kutoa elimu ya ujuzi kwa miaka 10; baada ya hapo mtoto akiona hawezi kuendelea, anaweza kujiajiri, na anayeendelea hadi chuo kikuu anaweza kuendelea na fani hiyo ya ufundi,” alisema Dkt. Niwagila.
Kwa upande wake, Meneja wa DC Polytechnic Education Institute College, Jackson Kailanga, alisema chuo hicho kinaendelea kutoa elimu katika fani mbalimbali kwa kuzingatia maboresho ya mtaala wa elimu yanayotekelezwa kupitia Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014 pamoja na maboresho yake ya mwaka 2023.
Alisema maboresho hayo yanaweka mkazo katika elimu inayozingatia stadi za kazi, vitendo na mahitaji ya dunia ya sasa.
Kailanga alisema chuo hicho kinatoa fursa kwa watu walioko kazini ambao hawakupata nafasi ya kuendelea na elimu ya juu kwa kuwajengea uwezo na kuwapatia maarifa yanayowawezesha kuendana na mahitaji ya elimu ya sasa.
Aliongeza kuwa walimu walioko mikoani huunganishwa katika vituo maalumu vya mafunzo ambapo hupatiwa wataalamu wa kuwafundisha hadi wanapohitimu masomo yao.
Aidha, alisema chuo hicho kinawakaribisha vijana waliomaliza darasa la saba hadi kidato cha nne kujiunga na mafunzo ya ufundi katika nyanja mbalimbali ikiwemo ufundi wa magari, umeme na taaluma nyingine za kiufundi. Alisema wataalamu kutoka vyuo vya ufundi stadi vya VETA hushiriki katika kuwajengea uwezo wanafunzi wanaojiunga na chuo hicho.
Alitoa wito kwa vijana kutokata tamaa kwani zipo fursa nyingi za kujiajiri kupitia ujuzi na ubunifu. Pia aliwataka walimu walioko kazini kuendelea kujifunza na kupokea maarifa mapya ili kukabiliana na mabadiliko yanayoendelea katika sekta ya elimu.
Naye Mkurugenzi wa Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (NACTVET) Kanda ya Ziwa, Godfrey Michael, alisema mhitimu bora ni yule anayeweza kutumia maarifa aliyoyapata kuijenga jamii yake na kuharakisha maendeleo.
Aliwataka wahitimu kutumia elimu waliyoipata kama nyenzo ya kuleta mabadiliko chanya katika jamii, kuongeza ujuzi unaohitajika kwa sasa, kuepuka vitendo vya rushwa na udanganyifu, na kuchangia utekelezaji wa mtaala mpya wa elimu nchini.
Na Mwandishi wetu - Dodoma
Mkurugenzi wa Idara ya Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Bi. Stella Mwaiswaga pamoja na Watumishi wengine kutoka Ofisi hiyo wameshiriki ufunguzi wa Maonesho ya Wiki ya Utumishi tarehe 17 Juni, 2026 katika viwanja vya Chinangali Park Jijini Dodoma.
Maonesho ya Wiki ya Utumishi ni moja ya matukio katika kalenda ya Umoja wa Afrika (AU) ambapo nchi wanachama huadhimisha kwa kaulimbiu moja na kufanya maonesho ya kazi mbalimbali kuhusu masuala ya Utumishi wa Umma ambapo hufanyika kila mwaka kuanzia tarehe 16 hadi 23 Juni.
Kwa mwaka huu Maadhimisho hayo yamebeba kaulimbiu isemayo; “Kuchochea Uwajibikaji Jumuishi wa Huduma Endelevu”.
SAmbamba na hilo Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu inashiriki maonesho hayo huku ikitoa elimu mbalimbali kwa umma kuhusiana na shughuli za Wakala Serikali wa uchapishaji Tanzania, elimu kuhusu masuala ya Menejimenti ya Maafa, Watu wenye Ulemavu, Ufuatiliaji na Tathimini pamoja na Masuala ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi.


.jpeg)













.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)





.jpeg)



.jpeg)
.jpeg)


.jpeg)
.jpeg)


