Na FARIDA MANGUBE, MOROGORO 

Wakati vijana wengi wakikabiliwa na changamoto za maadili na msukumo  rika, Serikali imeidhinisha rasmi kitabu cha Dunia Yangu Bora kitakachotumika kufundisha stadi za maisha kwa wanafunzi wa sekondari katika halmashauri 76 za mikoa 10 nchini.

Hatua hiyo inaashiria upanuzi wa utekelezaji wa programu hiyo iliyokuwa ikitumika katika halmashauri 35 pekee kabla ya kuongezwa halmashauri 41 zaidi, na hivyo kufikia jumla ya halmashauri 76.

Mkuu wa Idara ya Miradi kutoka Campaign for Female Education (CAMFED), Bi Dominica Lyambo, amesema kabla ya ithibati rasmi, kitabu hicho kilikuwa kikitumika kwa majaribio katika baadhi ya halmashauri, lakini sasa kitapewa wigo mpana zaidi baada ya kuidhinishwa na Serikali.

Lyambo amesema lengo la kitabu hicho ni kuwajengea wanafunzi uwezo wa kujitambua, kuelewa sababu za kuwa shuleni na namna ya kukabiliana na changamoto za maisha.

“Ni stadi za maisha zinazomsaidia mwanafunzi kuelewa kwa nini yupo shuleni, kwa nini anapaswa kusoma, changamoto zilizopo katika jamii na namna ya kuzikabili ili kufikia ndoto zake,” alisema Lyambo.

Aliongeza kuwa utekelezaji wa programu hiyo unatarajiwa kuongeza mahudhurio ya wanafunzi shuleni na kuboresha kiwango cha ufaulu.

Kwa mujibu wa CAMFED, mpango wao ni kuhakikisha ifikapo mwaka 2030 wanafikia angalau asilimia 85 ya halmashauri zote za wilaya katika mikoa 26 ya Tanzania Bara, kutoka mikoa 10 iliyofikiwa kwa sasa.

Lyambo alisisitiza kuwa programu hiyo inawahusisha wanafunzi wote wa kidato cha kwanza na cha pili  wavulana na wasichana  na utekelezaji wake utakuwa endelevu. 

Katika utekelezaji wake, kila halmashauri imeteua walimu wawili hadi wanne watakaopatiwa mafunzo maalum, kisha kuwafundisha wawezeshaji wengine watakaosimamia mafunzo hayo ngazi ya shule.

Akizungumzia upekee wa kitabu hicho, Lyambo alisema tofauti na vitabu vya masomo ya darasani, Dunia Yangu Bora kinajikita katika ustawi wa binafsi, maadili, uwezo wa kujisimamia na kukabiliana na changamoto za kihisia na kijamii.

Kwa upande wake, Afisa Mwandamizi kutoka Ofisi ya Kamishna wa Elimu, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Fredy Nyandoro, amesema kitabu hicho kimepewa ithibati kama kitabu cha ziada chenye maudhui ya stadi za maisha yanayokamilisha masomo ya kawaida.

Amesema maudhui yake yanawalenga vijana wa Kitanzania walioko katika umri wa balehe kwa kuwajenga katika misingi ya uadilifu, uwajibikaji, kujituma, upendo, utu na utunzaji wa mazingira.

“Dunia ya sasa inawakabili vijana na changamoto nyingi za kuporomoka kwa maadili. Kitabu hiki kinamjenga kijana kuipenda na kuitunza dunia yake, kuelewa mchango wake katika jamii na kushiriki kutatua changamoto,” alisema.

Aliongeza kuwa kitabu hicho kinatumia visa na hadithi zinazoonesha namna ya kushirikiana na wazazi, marafiki na jamii katika kutatua changamoto, huku kikisisitiza kuwa hakuna kukata tamaa katika maisha.

Akizundua kitabu hicho Mwakilishi wa Kamishna wa Elimu nchini, Dkt. Gladness Kirei, amezitaka halmashauri 76 zilizoanza kutekeleza programu hiyo kuwa na mpango kazi madhubuti wa kuhakikisha elimu ya stadi za maisha inatekelezwa kikamilifu mashuleni.

Pia amewataka maafisa elimu kata kufuatilia utekelezaji wake kwa kukusanya takwimu za mahudhurio na kufanya tathmini ya ufundishaji, huku akisisitiza umuhimu wa kuwashirikisha wazazi kupitia mikutano na semina za uelimishaji.

“Mafanikio ya mradi huu hayatapimwa kwa idadi ya vitabu vilivyosambazwa au walimu waliopatiwa mafunzo, bali kwa mabadiliko ya kitabia kwa vijana, ongezeko la mahudhurio, kupungua kwa mimba za utotoni na kuimarika kwa ufaulu,” alisema Dkt. Kirei.

Kwa upande wao walimu walioshiriki katika uzinduzi huo wameishukuru serikali kwa kutoka Ithibati ya kitabu hicho kwani kimekuwa nguzo muhimu katika kubadilisha maisha ya wanafunzi katika kujitambua.




Na WMJJWM – Dodoma

Serikali imetoa mwongozo rasmi wa maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Wanawake kwa mwaka 2026, yatakayofanyika kuanzia Machi 1 hadi 8 kote nchini.

Hayo yamebainishwa Februari 17, 2026 na Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima, wakati akizungumza na vyombo vya habari jijini Dodoma, ambapo amesema maadhimisho hayo yatafanyika kuanzia ngazi ya kijiji hadi mkoa yakiongozwa na mwongozo maalum uliotolewa na Wizara.

Waziri Dkt. Gwajima amesema kuwa kaulimbiu ya maadhimisho ya mwaka 2026 ni “Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana: Msingi Jumuishi kufikia Dira 2050”, ikilenga kujenga uelewa wa kuwekeza katika maendeleo jumuishi kwa kutambua na kutekeleza haki za wanawake na wasichana kwa vitendo.

Amesisitiza kuwa kaulimbiu hiyo imejikita katika nguzo za Dira ya Taifa ya 2050 na inahusisha makundi yote ya kijamii.

Katika mwongozo huo, Waziri Dkt. Gwajima ameeleza kuwa kila mkoa utawajibika kuratibu maadhimisho na kutoa taarifa kwa umma kuhusu ratiba na maudhui ya shughuli zitakazofanyika. Aidha, sare rasmi ya maadhimisho itakuwa vazi la batiki, ambapo kila mkoa utahamasishwa kutumia wazalishaji wa ndani ili kuinua uchumi wa wajasiriamali wa ndani, hususan wanawake.

Amefafanua kuwa maadhimisho ya mwaka huu yanajengwa juu ya misingi ya Ulingo wa Beijing wa mwaka 1995 unaolenga kukuza usawa wa kijinsia na uwezeshaji wa wanawake kupitia ajenda 12 muhimu, ikiwemo kupinga umaskini, ukatili wa kijinsia, kuboresha afya na elimu, pamoja na kuongeza ushiriki wa wanawake katika uongozi na uchumi.

Aidha, amesema maadhimisho hayo yatahusisha midahalo, makongamano, maonesho ya wajasiriamali, uzinduzi wa miradi ya kijamii, mashindano ya kielimu na michezo ya kuelimisha, utoaji wa tuzo kwa wanawake vinara pamoja na matembezi ya hiari siku ya kilele. Pia, wananchi wataelimishwa kuhusu huduma za msaada wa kisheria, uwezeshaji wa kiuchumi na maadili ya jamii.

Waziri Dkt. Gwajima amesisitiza kuwa maadhimisho hayo hayahusiani na itikadi yoyote bali ni ya wanawake wote kwa kushirikiana na wanaume kama wadau wakuu wa maendeleo. Amevitaka vyombo vya habari kutoa ushirikiano ili kuhakikisha taarifa za maadhimisho zinawafikia wananchi wote, huku akibainisha kuwa Wizara itaungana na Mkoa wa Geita katika maadhimisho hayo na tathmini ya ushiriki wa mikoa itatolewa Machi 30, 2026.








-Akagua na kuzindua shule ya sekondari ya amali Majulai, Lushoto  

WAZIRI MKUU Dkt Mwigulu Nchemba amewaagiza baadhi ya mawaziri alioambatana nao wabakie mkoani Tanga ili kufuatilia masuala yaliyoibuliwa na wananchi na kuyatafutia ufumbuzi. 

Masuala hayo yalitokana na hoja zilizoibuliwa kwenye mikutano ya hadhara na wabunge wa mkoa wa Tanga na wananchi mbalimbali kwenye sekta za ardhi, mifugo, kilimo, maji, elimu na barabara. 

Ametoa agizo hilo leo (Jumanne, Februari 17, 2026) wakati akizungumza na wakazi wa Soni, Bumbuli katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye stendi ya Soni, wilayani Lushoto, mkoani Tanga.

Mapema, akijibu hoja kuhusu ubovu wa barabara wilayani Lushoto, Naibu Waziri wa Ujenzi, Mhandisi Godfrey Kasekenya alisema Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameshatoa kibali cha kuanza ujenzi wa pande mbili wa barabara ya Soni - Bumbuli- Dindira hadi Old Korogwe. 

“Barabara hii ilishatangazwa na sasa tunakamilisha taratibu za wakandarasi. Zikiwa tayari, mmoja ataanzia Soni kwa kujenga kilometa 22 na mwingine ataanzia Old Korogwe (KwaMeta hadi KwaShemsi) kwa kujenga kilometa 9.5,” alisema.

Alisema barabara ya sasa ya kutoka Mombo - Soni hadi Lushoto yenye urefu wa km. 32 imeshafanyiwa usanifu na inatafutiwa fedha ili iweze kufanyiwa upanuzi.

Naye Naibu Waziri wa Kilimo, David Silinde alisema Msajili wa Hazina anamalizia uhakiki wa madeni ya zamani ya wakulima wa chai waliokuwa wanadai malipo katika kiwanda cha chai cha Mponde na kuongeza kuwa katika kipindi cha hivi karibuni hakuna madeni yoyote yaliyolimbikizwa.

Alisema kiwanda hicho ambacho kinahudumia Halmashauri mbili za Bumbuli na Korogwe, kinafanyiwa mpango wa kupata line nyingine ya uzalishaji ili kupunguza mlundikano wa majani ya chai yaliyovunwa. Alisema Bodi ya Chai imeshanunua kiwanda kingine huko Korogwe ambacho kinatarajiwa kuanza kazi kabla ya Juni, mwaka huu ili kisaidie kupunguza mzigo unaoenda kiwanda cha Mponde.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amekagua na kuzindua shule mpya ya sekondari ya amali ya Majulai iliyopo katika kijiji cha Majulai, Kata ya Mwangoi, Tarafa ya Mlalo wilayani Lushoto.

Shule hiyo ambayo imejengwa kwa kupitia mradi wa SEQUIP na tayari imesajiliwa, ina walimu sita na wanafunzi 89 ambao walianza masomo Januari 13, 2026..

Akitoa taarifa ya ujenzi wa shule hiyo, Mkuu wa shule ya Sekondari Shita ambayo ni shule mama, Mwalimu Ramadhani Mohammed alisema mradi huo ambao umegharimu sh. milioni 584.28 ulianza kutekelezwa Oktoba 23, 2024 na hadi sasa umetumia sh. milioni 581.81 na kwamba sh. milioni 2.46 zilizobakia ni za angalizo, kukamilisha ujenzi wa tenki na kulipa mafundi.




Shirika la Reli Tanzania (TRC) limeanza rasmi usafirishaji wa makasha kwa kutumia reli ya Standard Gauge, hatua inayolenga kupanua wigo wa biashara, kupunguza msongamano wa mizigo bandarini na kurahisisha usafirishaji wa mizigo kwenda mikoa ya kati ya nchi.

Akizungumza wakati wa kuanza safari ya treni ya kwanza ya makasha kutoka Pugu kuelekea Ihumwa mkoani Dodoma, Kaimu Mkurugenzi wa Usafirishaji wa TRC, Focus Makoye Sahani, amesema treni hiyo inasafiri umbali wa takribani kilometa 420 kutoka Dar es Salaam.

Amesema hatua hiyo ni mwanzo wa usafirishaji wa makasha baada ya TRC kuanza kusafirisha abiria pamoja na mizigo mbalimbali ikiwemo kichele kuanzia mwezi Julai, pamoja na saruji inayopakiwa Pugu.

“Leo tumeongeza wigo wa biashara kwa kupakia makasha. Kama mnavyoona, treni yetu ya kwanza ya makasha kwenda Ihumwa, Dodoma, leo imeanza safari zake na tuna ofa ya kutosha kutoka kwa mteja wetu wa kwanza,” amesema Sahani.

Ameeleza kuwa treni hiyo ina mabehewa 50 yanayobeba jumla ya makasha 100, huku mteja wa kwanza, GSM, akitoa ofa ya kuanzia kwa huduma hiyo.

Kwa mujibu wa Sahani, TRC imeanza upakiaji wa makasha katika eneo la Pugu, huku ikifanya maboresho ya miundombinu ikiwemo Malindi Yard karibu na eneo la Gerezani  ili kuimarisha shughuli za upakiaji wa makasha.

Ameeleza kuwa hatua hiyo itasaidia kupunguza msongamano wa mizigo bandarini, sambamba na utekelezaji wa maelekezo ya Mkurugenzi Mkuu ya kuhakikisha uwepo wa Vituo vya Kontena vya Ndani (ICD) katika Morogoro, na Ihumwa .

“Tutakuwa na ICD Morogoro ambayo ipo kilometa 193 kutoka Dar es Salaam, ambako wateja wanaoelekea Mbeya na Iringa wataweza kuchukua mizigo yao. Lakini pia kuna ICD ya Ihumwa ”amesema.

Ameongeza kuwa safari ya kuelekea Morogoro huchukua muda mfupi, huku mzigo unaoelekea Dodoma ukishushwa katika ICD ya Ihumwa, ambako kuna eneo kubwa na miundombinu ya kutosha kuhudumia makasha.

Akitoa wito kwa wafanyabiashara, Sahani amewahimiza Watanzania kutumia usafiri wa reli ili kupunguza utegemezi wa malori kutoka Dar es Salaam kwenda Dodoma, akisisitiza kuwa huduma ya reli ya Standard Gauge ni rahisi, salama na yenye ufanisi.

Hii ni mara ya kwanza kwa TRC kutumia container carries,  toka ilipoanza usafirishaji wa  mizigo kwa SGR Juni 27, 2026.

Shirika la Reli Tanzania (TRC) lilipokea jumla ya mabehewa 264 ya mizigo ya  SGR Desemba 2024 ambapo  kati ya hayo mabehwa 200 yakiwa ni ya kubebea makontena (containers carriers) na 64 ni ya kubebea mizigo isiyofungwa (loose cargoes).



Na FARIDA MANGUBE, MOROGORO.


Serikali kupitia Wizara ya Kilimo inampango kuanzisha zaidi ya vituo 1,000 vya kuhifadhi mashine za kilimo ili kurahisisha upatikanaji wake kwa wakulima na kuongeza uzalishaji.

Hayo yalisemwa na Naibu Katibu Mkuu (Maendeleo ya Mazao na Usalama wa Chakula) wa Wizara ya Kilimo, Profesa Peter Msoffe, mjini Morogoro alipomwakilisha Katibu Mkuu wa wizara hiyo katika jukwaa la kubadilishana uzoefu kati ya Tanzania na Japan kupitia Japan International Cooperation Agency (JICA), kwa kushirikiana na Sokoine University of Agriculture (SUA).

Profesa Msoffe amesema mafanikio ya mageuzi ya kilimo hayawezi kupatikana bila kuwekeza katika kilimo cha kisasa kinachotumia mashine badala ya kutegemea nguvu kazi ya mikono.

Ameleza kuwa vituo hivyo vitahusika na kuhifadhi na kufanya matengenezo ya mashine, pamoja na kuhakikisha zinapatikana kwa urahisi kwa wakulima.

Amesema dhamira ya Serikali ya kuboresha kilimo si ya maneno bali ni ya vitendo, akibainisha kuwa tayari hatua za kuanzisha vituo hivyo zimeanza sambamba na utoaji wa ruzuku ya mbolea na pembejeo mbalimbali kwa wakulima.

Akizungumzia uzoefu wa Japan katika kuendeleza kilimo cha kisasa, Profesa Msoffe alisema Tanzania ina mengi ya kujifunza, akifananisha ushirikiano huo na darasa muhimu kwa wataalamu wa kilimo nchini.

Jukwaa hilo, ambalo limekuwepo kwa takribani miaka minne, linawakutanisha wataalamu kutoka Tanzania na Japan kujadili na kubadilishana uzoefu kuhusu matumizi ya teknolojia na mashine katika sekta ya kilimo.

“Kama mnavyofahamu, Tanzania inapitia mabadiliko makubwa katika sekta ya kilimo. Baada ya kupitishwa kwa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, nchi imejipanga kuongeza kasi ya maendeleo ya kiuchumi na kufikia uchumi wa takribani dola trilioni moja ifikapo mwaka 2050, huku kipato cha mwananchi kikitarajiwa kufikia wastani wa dola 7,000,” alisema.

Kwa upande wake, Mwakilishi Mkuu wa JICA nchini Tanzania, Ara Hitoshi, alisema ushirikiano kati ya JICA na SUA ulianza mwaka 2022 ukiwa na lengo la kushirikiana katika maendeleo ya sekta mbalimbali, hususan kuwawezesha vijana.

Amesema kilimo ni sekta muhimu kwa uchumi wa Tanzania na kupitia jukwaa hilo vijana watanufaika kwa kujifunza namna Japan inavyotumia mashine na teknolojia za kisasa katika uzalishaji badala ya kutegemea kilimo cha mazoea.

“Nafikiri kilimo ni sekta muhimu kwa Tanzania. Tunapenda kushirikiana katika programu hii ili wataalamu wa Japan na Tanzania wabadilishane uzoefu, hususan kwa kuwalenga vijana katika matumizi ya teknolojia za kisasa,” alisema.

Afisa Mwandamizi wa Sayansi, Teknolojia na Ubunifu kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Edwin Konzo, alisema ili kufikia malengo ya Dira ya 2050 kuna haja ya kufanya mapitio ya sera mbalimbali, ikiwemo Sera ya Sayansi na Teknolojia ya mwaka 1996, ili iendane na mahitaji ya sasa.

Amesema sekta ya kilimo ni injini muhimu ya mabadiliko ya kiuchumi na mafanikio yake yanategemea matumizi ya teknolojia na ubunifu.

“Mkutano huu unalenga kujifunza kutoka kwa teknolojia zilizotumiwa na Japan katika mageuzi ya kilimo, ili wataalamu wetu waweze kutumia maarifa hayo kuboresha uzalishaji, kuendeleza mbegu zenye ustahimilivu na kuongeza faida kwa wakulima,” alisema.

Naye Naibu Makamu Mkuu wa SUA (Utawala, Fedha na Mipango), Profesa Amandus Muhairwa, alisema jukwaa hilo linatoa fursa kwa Watanzania kujifunza kutoka kwa Wajapani kuhusu uhandisi na teknolojia katika kilimo.

Ameongeza kuwa wakati vijiji vingi vikibadilika na kuwa miji, eneo la ardhi linalopatikana kwa kilimo linapungua, hivyo kuna haja ya kuongeza tija katika uzalishaji, si tu katika kilimo bali pia katika sekta ya ufugaji.





Na Mwandishi Wetu


MAMLAKA ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) kwa kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama kukamata kilogramu 299.8 za dawa za kulevya aina ya mirungi pamoja na kuteketeza ekari 203 za mashamba ya mirungi.

Ukamati wa dawa hizo umetokana na ushirikiano kati ya Mamlaka hiyo na vyombo Vya Ulongoniz na usalama hususan Jeshi la Polisi, baada ya kufanya operesheni maalum iliyoanza Februari 10 hadi 16 Februari, 2026 katika vijiji vya Marieni na Mhero vilivyopo kata ya Chome, wilaya ya Same, Kilimanjaro na kufanikiwa

Akizungumza mara baada ya operesheni hiyo, Kamishna Jenerali wa DCEA, Aretas Lyimo amesema, watu saba wamekamatwa kuhusiana na uhalifu huo.

Aidha ameongeza kuwa, licha ya jitihada za muda mrefu za utoaji elimu na operesheni za mara kwa mara, bado kuna watu wachache wanaoendelea kukaidi sheria za nchi.

“Serikali imefikisha huduma muhimu ikiwemo umeme na maji safi pamoja na miradi ya kilimo na ufugaji. Wananchi wengi wameanza kujishughulisha na mazao mbadala kama vile vitunguu, viazi, kabeji, parachichi na kahawa,” amesema Kamishna Jenerali Lyimo.

Pia amesisitiza kuwa, Mamlaka itaendelea kushirikiana na viongozi wa vijiji, kata, wilaya na mkoa pamoja na wadau wengine kutoa elimu na kutekeleza operesheni endelevu ili kuhakikisha tatizo la mirungi linadhibitiwa kikamilifu katika mkoa wa Kilimanjaro.

Kwa upande wake Mtendaji wa Kijiji cha Mhero, Hamad Waziri Hamad, amesema operesheni hiyo itakuwa msaada mkubwa katika kijiji hicho kwa sababu itasaidia vijana wengi kuachana na kilimo na matumizi ya mirungi, kwani madhara yalikuwa mengi kwa vijana ikiwemo vitendo vya uhalifu na kuhatarisha usalama wa wakazi wa maeneo hayo.

Nao baadhi ya wakazi wa Chome akiwemo, Rafael Kisenge mkulima wa mazao mseto wamethibitisha uwepo wa fursa zilizopo katika maeneo hao ikiwemo ardhi yenye rutuba inayostawisha mazao halali.

“Naishukuru serikali kwa kuweka mfumo mzuri, tunapata ruzuku ya pembejeo na hata tukilima katika eneo dogo tumekuwa tukipata faida. Hivyo hakuna sababu za kufanya kilimo haramu” amesema Kisenge.

Kadhalika, Mohamed Athuman Mbwabo mkazi na dereva wa maroli amesema, kufuatia operesheni zilizofanyika baadhi ya wakazi wa maeneo hayo wameachana na kilimo cha mirungi na wachache waliokaidi, wamekamatwa na kuchukuliwa hatua za kisheria.

Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya inatoa wito kwa wananchi kuendelea kushiriki katika mapambano dhidi ya dawa za kulevya kwa maendeleo ya jamii na Taifa kwa ujumla.





Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Festo Dugange amesema ushirikiano wa Tanzania Bara na Zanzibar ni nguzo muhimu katika kukabiliana na athari za mazingira.

Amesema hayo wakati wa kikao cha ushirikiano kati ya Ofisi ya Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (SJMT) na Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) kilichofanyika leo Februari 17, 2026, Zanzibar.

Katika kikao hicho ngazi ya Mawaziri, Dkt. Dugange ambaye ni Mwenyekiti Mwenza alihimiza ushirikiano madhubuti baina ya Ofisi ya Makamu wa Rais na Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais katika utekelezaji wa shughuli za kimazingira ambao utasaidia katika kukabiliana na changamoto za uharibifu wa mazingira.

Alisema suala la mazingira halina mipaka linaihusu Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hata kama changamoto zinatokea nje ya mipaka ya taifa bado SJMT na SMZ zinashirikiana kwa karibu katika kuweka mazingira vizuri.

“Lazima tushikamane mara kwa mara kuhusu masuala ya biashara ya kaboni mazingira, chochote cha Bara na Zanzibar lazima tuongee lugha moja, hatuwezi kufanya vizuri sana kama hatushirikiani, hivyo niwapongeze Makatibu Wakuu kwa kuona umuhimu wa kukutana na kujadili masuala ya mazingira na kufikia malengo,” alisisitiza.

Hivyo, Naibu Waziri alitoa rai kwa wajumbe wa kikao hicho kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais na Ofisi ya Makamu wa Kwanza hicho kuyafanyia kazi yale yote yaliyoafikiwa katika kikao cha ngazi ya Makatibu Wakuu.

Kwa upande Wake Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais (Sera, Uratibu na Baraza la Wawakilishi) Mhe. Hamza Hassan Juma alishauri elimu ya Muungano iendelee kutolewa hususan kwa kundi la vijana.

Alishauri kuwatumia wasanii mbalimbali nchini katika kutoa elimu ya Muungano, kwani wengi wao ni vijana hatua itakayoisaidia kufikisha ujumbe kwa haraka zaidi katika kundi hilo. 

Halikadhalika, Mhe. Hamza alitoa rai kwa watendaji kutoka Ofisi hizo mbili kutangaza zaidi fursa zinazopatikana katika Muungano badala ya changamoto akisema kuwa Serikali zote zinazishughulikia ili kuzimaliza.

Awali akizungumza wakati wa kikao cha ushirikiano ngazi ya Makatibu Wakuu, Kwa upande wake Kaimu Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Bw. Ilyasa Pakacha Haji alisema kuwa kuna haja kubwa ya kuendeleza ushirikiano huo kukabiliana na athari za mazingira.

Alisema athari za mazingira hususan mabadiliko ya tabianchi yanagusa dunia na kuwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni mojawapo ya nchi ambazo zinakumbwa na changamoto hiyo.

Hivyo, vikao vya ushirikiano ni hatua nzuri ya kuandaa na kutekeleza mapendekezo yote yaliyotolewa ngazi ya Makatibu Wakuu, kisha kufuatilia na kufanya tahmini kutambua ni zipi changamoto na kuzifanyia kazi. 







Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imesisitiza dhamira yake ya kuendeleza Sekta ya elimu kwa kutambua na kuunga mkono juhudi za waandishi bunifu na wachapishaji wa ndani.

Akizungumza kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Mkurugenzi Msaidizi wa Usajili wa Shule Patrick Leana amesema kuwa washindi wa Tuzo ya Taifa ya Uandishi bunifu wameonyesha ubunifu na weledi wa hali ya juu na kwamba zawadi walizopokea ni sehemu ya kutambua mchango wao katika kukuza maarifa na utamaduni wa kusoma nchini.

Aidha, amewapongeza wachapishaji wa kampuni za ndani kwa kuhakikisha vitabu vinachapishwa na kusambazwa kwa wakati, hatua inayowezesha wanafunzi na jamii kupata rasilimali bora za kujifunza.

"Pamoja na kuwapongeza wachapishaji, nitoe shukrani za dhati kwa kamati ya maandalizi na viongozi wote waliowezesha mchakato wa tuzo kwa mchango wao wa kitaaluma na kujitolea," ameongeza Mkurugenzi Leana.

Amesema kuwa ushiriki wa waandishi kutoka kada mbalimbali na maeneo tofauti, ndani na nje ya nchi, ni ushahidi wa hamasa kubwa ya kitaifa na kimataifa katika kukuza uandishi bunifu.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Elimu Tanzania (TET), Dkt. Anneth Komba, amesema kuwa Tuzo ya Taifa ya Mwalimu Nyerere ya Uandishi bunifu ni nyenzo muhimu ya kuibua na kukuza vipaji vya waandishi wa ndani.

“Mpango huu ni chombo cha kitaifa cha kutambua ubunifu na kuendeleza utamaduni wa Kiswahili kupitia maandiko ya waandishi chipukizi na waliobobea na kwamba hatua ya kusambaza vitabu kwa shule zote nchini inalenga kuimarisha utamaduni wa kusoma na kuongeza kiwango cha elimu” amesema Dkt. Komba

Amesema kuwa jumla ya nakala 120,000 za vitabu vitatu vya riwaya Biarasa, ushairi Mgoma ya Mwere, na hadithi za watoto Maziwa ya Kijiji vimechapishwa na vitasambazwa kwa shule na kueleza kuwa kila Shule itapata kati ya vitabu 8 hadi 10. 

Vitabu hivyo vitatumika kama rasilimali za maktaba na vinatarajiwa kusomwa na wanafunzi wengi, hatua inayoongeza upatikanaji wa maarifa na kuhamasisha kizazi kipya kupenda kusoma.

Amesema kuwa kiasi cha shilingi milioni 100 kilitengwa katika mwaka wa fedha 2024/2025 kwa ajili ya uchapishaji na usambazaji. Hatua hiyo imeelezwa kuwa ni sehemu ya mkakati wa kuhakikisha upatikanaji wa vitabu bora na kuimarisha uchumi wa maarifa nchini.






SHAHIDI wa tisa katika kesi hiyo, Ofisa wa Jeshi la Polisi ASP Geofrey Lutufye (47), ameieleza Mahakama kuwa vijana wawili waliokamatwa walikiri kushawishika na maneno ya Mwenyekiti wa Chadema, Tundu Lissu, na kuamua kuunga mkono wito wa kuzuia uchaguzi mkuu wa mwaka 2025.

Akiongozwa na Wakili wa Serikali Mwandamizi, Renatus Mkude, mbele ya jopo la majaji watatu linaloongozwa na Jaji Dunstan Ndunguru akishirikiana na Jaji James Karayamaha na Jaji Ferdinand Kiwonde, shahidi huyo alieleza kuwa watuhumiwa hao walikamatwa wakiwa katika kijiwe cha bajaji eneo la Mrombo, Arusha.

ASP Lutufye alidai kuwa Aprili 3, 2025, akiwa kwenye doria na kikosi chake chenye askari tisa wakitumia gari la polisi aina ya Toyota Land Cruiser, alipokea maelekezo kutoka kwa Kaimu Mkuu wa Upelelezi, ASP Bonny Mgogo, kwenda eneo hilo kufuatilia taarifa za vijana wanaopanga kuzuia uchaguzi.

“Nilipofika eneo la Mrombo nilikuta vijana wakila njama za kuzuia uchaguzi mkuu wa mwaka 2025,” alidai.

Alisema waliwakamata vijana wawili waliotajwa mahakamani kama P4 na P7 na kuwapeleka Kituo cha Polisi Murieti mkoani Arusha kwa hatua zaidi.

ASP Lutufye alieleza kuwa wakiwa njiani aliwahoji watuhumiwa hao kuhusu tuhuma hizo.

“Niliwauliza kwa nini wanahusika kula njama za kuzuia uchaguzi mkuu wa 2025. Wote walikiri kuwa wanamuunga mkono Mwenyekiti wa Chadema, Tundu Lissu, kutokana na kauli aliyoitoa mtandaoni kwamba atazuia uchaguzi, ataleta uchochezi na atakinukisha,” alidai shahidi huyo.

Mahakamani hapo, alieleza kuwa aliagizwa kuwapeleka watuhumiwa hao katika Ofisi ya Mkuu wa Upelelezi Mkoa na baadaye kuanzisha jalada la uchunguzi lenye namba ARS/D/CID/B/40/2025.

Aidha, alidai kuwa alipokea maelekezo ya kuwahoji zaidi watuhumiwa hao, maelekezo ambayo aliyatekeleza kwa kushirikiana na askari wengine, huku yeye akiandika maelezo yake ya ushahidi Aprili 18, 2025.

Kabla ya kueleza tukio hilo, ASP Lutufye aliitambulisha Mahakama kuhusu taaluma na uzoefu wake, akisema alihitimu mafunzo ya awali ya polisi katika Chuo cha Polisi Moshi Aprili 28, 2003 na kumaliza Novemba mwaka huo. Pia alipata mafunzo ya nyota ya kwanza mwaka 2013 katika chuo hicho, na baadaye mafunzo ya cheo cha Mrakibu Msaidizi wa Polisi katika Chuo cha Polisi Dar es Salaam (Police Academy), aliyohitimu Novemba 2023.

Alisema ana uzoefu wa miaka 15 katika majukumu ya upelelezi, akianzia Kituo cha Polisi Oysterbay jijini Dar es Salaam kama askari wa kawaida (general duty), kabla ya kuhamishiwa Ofisi ya Upelelezi wa Makosa ya Jinai Mkoa wa Geita na baadaye Mkoa wa Arusha, ambako kwa sasa ni kiongozi wa kikosi cha Anti Robbery.

Shahidi huyo alieleza kuwa majukumu yake ni pamoja na kufanya doria, kukamata watuhumiwa, kufanya upelelezi na kuwafikisha mahakamani.... Kesi inaendela
Na Hassan Kimweri, WAF - Manyara

Wizara ya Afya kwa kushirikiana na wadau kutoka Taasisi ya Elizabeth Glaser Pediatric AIDS Foundation (EGPAF) imefanya kikao kazi kwa lengo la kutathmini namna bora ya kuendeleza utoaji wa huduma bora za afya kufuatia kupungua kwa mchango wa wafadhili duiniani.

Akiongea wakati wa kikao hicho, Mganga Mkuu wa Serikali Dkt. Grace Magembe amesema kikao kimefanyika kwa wakati muafaka, hasa ikizingatiwa tayari wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wizara ya Afya ya kuchukua jukumu la kuandaa mpango mkakati wa uendelevu wa huduma za afya nchini.

"Huduma za afya ni lazima ziendelee kutolewa kwenye maeneo yote muhimu ikiwemo UKIMWI, Kifua Kikuu, Malaria, Afya ya Mama na Mtoto, Magonjwa Yasiyoambukiza usafirishaji wa sampuli na ajira za wataalamu wa sekta ya afya. licha ya mabadiliko ya ufadhili wa afua za Afya duniani, kote”amesema Dkt. Magembe

Dkt. Magembe amesema, Serikali imetoa kiasi cha shilingi bilioni 142 kama fedha za awali kwa ajili ya ununuzi wa dawa za kufubaza virusi vya UKIMWI (ARV), Kifua Kikuu, Malaria pamoja na vifaa vya uchunguzi, hatua inayolenga kuwa na uendelevu wa huduma.

Amezitaja hatua nyingine zilizochukuliwa ni kuandaa mpango wa uendelevu wa huduma (Sustainability Plan), kuanzishwa kwa Bima ya Afya kwa wote, kutoa huduma jumuishi (Integration of Health Services), kutenga vyanzo mahususi vya fedha za ndani kugharamia huduma za afya na kuimarisha mifumo ya kidijitali na huduma za afya ngazi ya msingi.

Pia amewapongeza wadau wa maendeleo, hususan EGPAF, kwa kuendelea kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuimarisha mifumo ya afya, akitolea mfano wa kazi iliyofanyika katika mkoa wa Manyara ambapo ziara ya vituo vya afya imeonesha mchango mkubwa wa wadau katika kuhakikisha huduma bora na endelevu zinawafikia wananchi.












-Aonya watendaji wa Serikali “kuzoea” matatizo ya wananchi

-Azindua mitambo ya kuzalisha hewa tiba ya Oksijeni


WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema kuwa anataka kuona kila fedha inayotolewa kwa ajili ya miradi ya maendeleo inatumika kama ilivyokusudiwa.

Amesema kuwa Serikali haiwezi kuvumilia kuona watendaji wa Serikali wenye dhamana wanashindwa kufuatilia matumizi ya fedha na kusababisha kushindwa kutekelezwa kwa miradi kwa viwango na ubora kwa manufaa ya wananchi.

Amesema hayo leo Jumanne (Februari 17, 2026) alipokuwa anazungumza na wananchi baada ya kuzindua mitambo ya kuzalisha hewa tiba ya Oksijeni katika Hospitali ya Wilaya ya Lushoto mkoani Tanga.

 Mradi huo ambao umegharimu kiasi cha shilingi milioni 526.8 una uwezo wa kuzalisha mitungi 120 ya kilo 50 kwa siku, hivyo kuboresha kwa kiasi kikubwa upatikanaji wa huduma hii muhimu.

Mitambo hiyo imeiwezesha Halmashauri kutolazimika kusafirisha mitungi ya oksijeni hadi Jijini Tanga umbali wa takribani kilometa 175 kwa ajili ya ujazaji. Hadi sasa, mtambo umefanikiwa kuzalisha mitungi 1,440 ya hewa tiba (oksijeni) ya kilo 50 na Mitungi 200 ya kilo 15.

 Aidha, Waziri Mkuu amewasisitiza watumishi wa umma kuhakikisha kutekeleza majukumu yao ipasavyo na si vinginevyo. “Tunataka watu wasilale ofisini, ninyi ni watumishi wa Serikali, fedha zikiletwa zikafanye kazi iliyokusudiwa.”

Mheshimiwa Dkt. Mwigulu amesema hayo wakati akihoji kuhusu kukosekana kwa ubora na viwango vya majengo, risiti za malipo, kutofanyika kwa kodi ya zuio, kukosekana kwa cheti cha ubora wa mabati, matofali na saruji katika baadhi ya shule za msingi wilayani humo.

 Kadhalika, Waziri Mkuu ameonya tabia ya baadhi ya watendaji wa Serikali kuwa na  utaratibu wa kuzoea matatizo ya wananchi. “Wapo baadhi ya watendaji wa Serikali wanapokea matatizo ya wananchi kama salamu na badala yake matatizo yanalimbikizwa sana.”








Top News