Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe Albert Chalamila amekutana na wahariri wa vyombo mbalimbali vya habari nchini ikiwa ni mkakati wa Mkoa huo kuimarisha uelewa kwa wananchi kuhusiana na usafi jijini humo, tahadhari ya mvua za Elnino, upangaji wa wafanyabiashara wadogo pamoja na maandalizi ya kupokea wanafunzi wa kidato cha kwanza mwaka 2018 

Akizungumza leo Septemba 17, 2026 jijini Dar es Salaam na wahariri wa vyombo vya Habari RC Chalamila amesema moja ya mambo ambayo Mkoa huo umekusudia kuyafanya ili kuimarisha usafi ni pamoja na kubadili mitazamo ya wananchi ili wawe na utamaduni wa kupenda kufanya usafi na kutenganisha taka kwa kutumia wataalamu kuelimisha jamii pamoja na kusimamia sheria za usafi ipasavyo

Chalamila amesema kuwa katika mkakati huo pia wametoa muda wa miezi mitatu kwa wakandarasi wa uzoaji taka kuwa na vifaa vya kisasa na teknolojia inayoendana na uhitaji wa Mkoa huo, sanjari na kuwezesha usafi kufanyika nyakati za usiku na kuwa na mifumo bora ya uondoshaji maji taka ambapo pia amezungumzia mpango wa kutumia taasisi binafsi kufanya uchakataji taka kupata mbolea na bidhaa zingine.

Akizungumzia suala la wafanyabiashara wadogo RC Chalamila amesema Mkoa huo imeweka mikakati bora ya kuhakikisha biashara ikiwemo za mama lishe zinafanyika kwenye maeneo rasmi na kuondoka maeneo yasio rasmi huku akielekeza TANROAD kuimarisha upandaji miti na utunzaji bustani za barabarani na ametoa muda wa wiki mbili kwa barabara ya uwanja wa ndege (Nyerere Road)

Aidha Mkuu wa Mkoa amezungumzia tahadhari ya uwepo wa Mvua za Elnino kama zilivyotabiriwa na mamlaka ya Hali ya Hewa Nchini TMA na kusema kuwa ni muhimu kwa wananchi kuendelea kuchukua tahadhari kwa kutoziba mitaro, kuepuka utupaji taka hovyo, kusafisha mito sanjari na kuhifadhi chakula huku akisisitiza kuwa s Mkoa huo unaendelea kuboresha miundombinu

Vilevile Chalamila ameeleza mikakati ya Mkoa huo kwa kushirikiana na wadau wa Sekta binafsi kukabiliana na uwepo wa idadi kubwa ya wanafunzi wa kidato cha kwanza mwaka 2018 kutokana na mabadiliko ya mitaala ambapo mwaka 2017 darasa la sita na la saba watahitimu hivyo mbali na ujenzi wa madarasa unaoendelea pia madarasa ya shule binafsi yatatumika

Kwa upande wa Mwenyekiti wa jukwaa la wahariri Tanzania TEF Deudatus Balile amezungumzia taarifa za kidunia zinazoashiria uwepo wa majanga ya mvua kubwa huku akisisitiza usimamizi wa sheria kwenye kuimarisha usafi wa mazingira.













Na Mwandishi Wetu

‎RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan, amepongezwa kwa kuwezesha Idara ya Uhamiaji kuendelea kuboresha na kuimarisha matumizi ya teknolojia za kisasa katika utoaji wa huduma za Uhamiaji, hatua inayolenga kurahisisha na kuongeza ufanisi katika taratibu za kuingia na kutoka nchini kwa raia na wageni.

Pongezi hizo zimetolewa na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Patrobas Katambi na Kamishna Jenerali wa Uhamiaji CGI Dkt. Anna Makakala wakati wa uzinduzi wa darasa la mafunzo ya mfumo huo katika Chuo Cha Uhamiaji Cha Kikanda TRITA Moshi Mkoani Kilimanjaro Septemba 2026.

‎‎Katika hatua hiyo ya mageuzi ya kidigitali, Idara ya Uhamiaji inatarajia kuanza kutumia mifumo mipya ya kiteknolojia katika vituo vya kuingia na kutoka nchini, ikiwemo Mfumo wa Advanced Passenger Information System (APIS) na Passenger Name Record (PNR).

‎Pia mifumo hiyo itawezesha upatikanaji na uchakataji wa taarifa za abiria kwa njia ya kidigitali kabla na wakati wa safari, jambo litakalosaidia maofisa uhamiaji kupata taarifa muhimu kwa wakati na hivyo kuwezesha huduma za uingiaji na utokaji nchini kutolewa kwa uharaka na ufanisi zaidi.

‎‎Aidha hatua hiyo ni sehemu ya jitihada za Serikali za kuendelea kuwekeza katika teknolojia na mifumo ya kisasa inayolenga kuboresha huduma kwa wananchi na wageni, huku ikiimarisha taratibu za usimamizi wa mipaka na usalama wa Taifa.

‎Kupitia maboresho hayo, Idara ya Uhamiaji Tanzania inaendelea kujikita katika matumizi ya teknolojia ya kidigitali ili kutoa huduma bora, salama, zenye ufanisi na zinazokwenda sambamba na viwango vya kimataifa.

‎Mifumo hiyo mipya inatarajiwa kuanza kufanya kazi hivi karibuni katika vituo husika vya kuingia na kutoka nchini.



Na Abdallah Nassoro - MOI
TAASISI ya Tiba ya Mifupa na Ubongo Muhimbili (MOI) imeanza kutumia technolojia ya kisasa kutoa matibabu ya kibingwa ya upasuaji wa ubongo kwa wagonjwa wa kiharusi inayongeza ufanisi wa matibabu Kwa wagonjwa.

Mkurugenzi wa Upasuaji wa Ubongo MOI Dkt. Lemeri Mchome amesema leo Septemba 17, 2026 kuwa technolojia hiyo ni ya kwanza kutumika nchini na kwamba inakwenda kuleta mapinduzi katika matibabu ya kiharusi.

"Tunatoboa tundu ndogo kichwani na tunapitisha kifaa maalum chenye kamera, Ile kamera inakwenda kutuonyesha eneo ambalo damu imevilia na kutuwezesha kuitoa bila kuathiri sehemu nyingine" amesema Dkt. Lemeri

"Hii ndiyo teknolojia ya kisasa zaidi duniani na sisi kama taasisi hatuko nyuma, wagonjwa wa kiharusi hawana sababu ya kukimbilia nje ya nchi Kwa matibabu, huduma hiyo inapatikana MOI...kwasasa tunapokea wagonjwa watatu hadi watano Kwa siku, teknolojia hii inakuwa msaada wa matibabu bora" ameongeza

Naye Daktari bingwa wa Upasuaji wa Ubongo MOI, Dkt. John Mtei ambaye ameshiriki katika upasuaji wa kwanza kwa kutumia kifaa hicho amesema technolojia hiyo inaacha alama katika mapinduzi ya tiba ya Kiharusi nchini.

"Ufanisi wa matibabu ndiyo nyenzo muhimu katika matumizi ya technolojia hii, mgonjwa anafanyiwa upasuaji na kuondolewa tatizo lake kwa uhakika" amesema Dkt. Mtei

Taasisi ya MOI imeendelea kujikita katika kuleta afua mbalimbali hapa nchini za kuipunguzia Serikali mzigo wa kupeleka wagonjwa nje ya nchi kwa rufaa za gharama kubwa na pia kuendelea kuwa kituo cha weledi cha matibabu ya Mifupa na mfumo wa fahamu barani Afrika





MWENYEKITI wa Chama cha Wamiliki wa Mabasi Tanzania (TABOA), Abdallah Kiongozi, amesema kuingia kwa mabasi ya King Long katika soko la Tanzania ni fursa ya kuimarisha sekta ya usafirishaji kupitia teknolojia, ubora na ushindani.

Kiongozi amesema mabasi yanayoletwa katika soko la Tanzania yanapaswa kuzingatia mazingira ya barabara nchini, safari za masafa marefu, uimara, matumizi bora ya mafuta pamoja na kutoa huduma salama na yenye starehe kwa abiria.

Amesema usalama wa abiria unapaswa kupewa kipaumbele, huku akieleza kuwa ubora wa uhandisi, viwango vya usalama, teknolojia na muundo wa kisasa ni mambo muhimu kwa mabasi yanayolenga kuhudumia soko la Tanzania.

“Gharama za mafuta ni miongoni mwa gharama kubwa kwa kampuni za mabasi. Hivyo, basi lenye matumizi mazuri ya mafuta na utendaji mzuri linaweza kusaidia kupunguza gharama za uendeshaji na kuongeza ufanisi wa biashara,” amesema Kiongozi.

Aidha, ameitaka King Long kuwekeza katika huduma baada ya mauzo, ikiwemo vituo vya matengenezo, upatikanaji wa vipuri na wataalamu wa kiufundi nchini, huku akisisitiza umuhimu wa kampuni kusikiliza maoni na mahitaji ya wamiliki wa mabasi ili kuboresha huduma zake.

Kiongozi pia ameshauri kuanzishwa kwa mifumo rafiki ya upatikanaji wa fedha kwa wamiliki wa mabasi kwa kushirikiana na taasisi za fedha nchini, akisema si rahisi kwa waendeshaji wengi kulipa gharama yote ya basi kwa wakati mmoja. Amesema iwapo King Long itaunganisha ubora wa mabasi, dhamana, vipuri, huduma baada ya mauzo na uwezeshaji wa kifedha, itakuwa na nafasi ya kujenga uhusiano mzuri na waendeshaji wa usafirishaji nchini.

Kampuni ya usafirishaji ya Rasco imeeleza kuwa imekuwa ikitumia mabasi ya King Long tangu mwaka 2018, ikibainisha kuwa katika kipindi hicho imejionea ubora, uimara, starehe na ufanisi wa mabasi hayo katika huduma za usafirishaji.

Mwakilishi wa kampuni hiyo amesema kwa waendeshaji wa usafirishaji wa abiria, uchaguzi wa basi ni uamuzi muhimu unaozingatia ubora, usalama, uimara na uwezo wa gari kufanya kazi kwa ufanisi katika safari mbalimbali.

Amesema tangu waanze kutumia mabasi hayo, wameendelea kushuhudia maboresho yanayofanywa na King Long kupitia ubunifu na teknolojia ili kuendana na mahitaji ya sekta ya usafirishaji.

Ameongeza kuwa Rasco inajivunia kuhusishwa na chapa hiyo na kutambua mchango wake katika kukuza huduma za usafirishaji, hususan kwa kutoa mabasi yenye starehe na yanayokidhi mahitaji ya safari za masafa marefu.

Kwa mujibu wa mwakilishi huyo, uzoefu wa Rasco wa kutumia King Long kwa miaka kadhaa unaonyesha uimara na utendaji wa mabasi hayo, jambo linalowapa waendeshaji msingi wa kuzingatia ubora na ufanisi wanapofanya maamuzi ya ununuzi wa mabasi.

Amesema mabasi yanayotoa huduma bora, salama na yenye starehe yana umuhimu mkubwa katika kuhakikisha abiria wanafanya safari zao kwa usalama na faraja.

Kwa upande wake, Meneja Mauzo wa Kampuni ya King Long, Ally Bakari Mkali, amesema kampuni hiyo imejipanga kutoa huduma bora baada ya mauzo kwa wamiliki wa mabasi nchini Tanzania, ikiwamo msaada wa kitaalamu, matengenezo na upatikanaji wa vipuri halisi.

Akizungumza katika uzinduzi wa chapa hiyo nchini, Mkali amesema uhusiano na mteja hauishii katika ununuzi wa basi, bali unaendelea kupitia huduma za matengenezo na msaada wa kitaalamu. Amesema King Long inalenga kushirikiana na wataalamu wa ndani pamoja na wamiliki na waendeshaji wa mabasi ili kuhakikisha huduma na bidhaa zake zinaendana na mahitaji ya soko.

Amesema kampuni hiyo inalenga kuwa mshirika wa muda mrefu katika sekta ya usafirishaji Tanzania na Afrika Mashariki, kwa kutoa magari yenye uimara, usalama na faraja kwa wasafiri. Ameongeza kuwa mrejesho kutoka kwa wadau utasaidia kuboresha bidhaa na huduma, huku uzinduzi huo ukiwa mwanzo wa ushirikiano mpana zaidi katika soko la Tanzania.


















Na Mwandishi wetu, Simanjiro 

MDAU wa maendeleo wa Mkoa wa Manyara, Taiko Kulunju Ole Tipa ameongoza harambee na kupatikana shilingi milioni 17 laki mbili na Elfu 27 na dume moja la ng'ombe ili kuwawezesha kiuchumi wanawake wa jamii ya wafugaji kikundi cha Enyoroto kijiji cha Kimotorok Kata ya Loiborsiret, Wilayani Simanjiro.

Taiko akizungumza kwenye harambee hiyo amesema wanawake hao wa kikundi cha Enyoroto wanapaswa kuwezeshwa kwani wana mchango mkubwa kwa jamii na ukimuwezesha mwanamke umeiwezesha jamii.

"Mama zetu wa jamii ya kifugaji wamebadili maisha yao kiuchumi na familia za hivyo tunawawezesha pia kuunga mkono jitihada za Rais wetu mpendwa Dkt Samia Suluhu Hassan ambaye amekuwa mstari wa mbele kusaidia jamii," amesema Taiko.

Amesema wanawake wa Simanjiro wamekuwa wakipambana kuichumi kwa maslahi mapana ya wao wenyewe, familia zao, jamii na Taifa kwa ujumla hivyo wanapaswa kuungwa mkono.

Mwenyekiti wa Kijiji cha Kikotorok, Elias Parmelo, ametoa shukrani za dhati kwa mdau wa maendeleo Taiko kwa jitihada na moyo wake wa kujitolea katika kusaidia shughuli mbalimbali za maendeleo zinazolenga kuboresha maisha ya watu

Parmelo amepongeza namna Taiko Kulunju anavyoendelea kushirikiana na jamii kwa vitendo, akieleza kuwa mchango wake ni mfano wa uzalendo, mshikamano na kujali maendeleo ya wananchi.

“Tunamshukuru sana Taiko Kulunju kwa moyo wake wa kusaidia jamii, tunathamini kazi anayofanya na tunaomba Mungu aendelee kumpa nguvu, afya na uwezo wa kuendelea kuwa sehemu ya maendeleo ya Kimotorok na jamii kwa ujumla,” amesema Parmelo. 

Katibu wa UWT Wilaya ya Simanjiro, Tichomo in Sangija amesema kutokana na mchango huo mkubwa wa Taiko, wanawake wa jamii ya kifugaji wa Kimotorok wameanza kubadili maisha yao kiuchumi kwa kupata fursa za uwezeshaji.

"Hatua hii ya uwezeshaji inasaidia kuongeza kipato na kujenga uwezo wa kujitegemea katika familia zao kwani kwa muda mrefu, wanawake katika jamii za wafugaji wamekuwa wapambanaji," amesema Sangija.

Mmoja kati ya wanufaika wa Enyoroto Esupat Solomon amesema wamekuwa wakishiriki katika shughuli mbalimbali za uzalishaji, ikiwemo ufugaji, biashara ndogo ndogo ila changamoto za ukosefu wa mtaji zimekuwa kikwazo hivyo uwezeshaji wa Taiko utawasaidia zaidi.



Na Victor Masangu,Kibaha 

Katika kuunga mkono juhudi za Rais wa awamu ya sita Dkt.Samia Suluhu Hassan katika kuboresha sekta ya elimu Mstahiki Meya wa Halmashauri ya  Manispaa ya Kibaha ameahidi kuimarisha mazuri ya ufundisha  kwa kujenga ofisi ya walimu katika shule ya Msingi Zegereni.

Hayo ameyabainisha  wakati wa mahafali ya pili ya Shule ya Msingi Zegereni iliyopo Kata ya Visiga, iliyopo katika  Manispaa ya Kibaha na kuhudhuliwa na viongozi mbali mbali wakiwemo wazazi pamoja na walezi

Amebainisha kwamba lengo lake kubwa ni kuweka mikakati madhubuti ya kuwasaidia walimu wawe na mazingira mazuri ya ufundishaji na kuondokana na changamoto ya kutokuwa na ofisi.

"Hawa watoto wetu ni tunu ya Taifa kwa hivyo wanapaswa kupatiwa misingi mizuri ya elimu ndio maana katiks hili nitahakikisha walimu wetu wanakuwa na ofisi nzuri ambazo zitawasaidia katika utekelezaji wa majukumu yao ya kuboresha elimu,'alisema Mstshiki Meya.

Pia Dkt Nicas amesema, wanafunzi wanatakiwa kuwa wazalendo  pamoja na kusoma kwa bidii ili kufikia malengo yaliyowekwa na serikali ya elimu ya lazima kuwa ni  kidato cha nne. 

"serikali ya Dkt Samia imelenga katika kuona miundo mbinu ya  elimu inaboreshwa zaidi na kuhakikisha wanafunzi wanasoma kwenye mazingira mazuri na wanapata elimu inayostahili", amesema Dkt Nicas.

Amesema, kila  mwanafunzi anawajibika kwa nafasi yake ili aweze kufanya vizuri kwenye masomo yao kwa sababu taifa linawategemea. 

Dkt Nicas ameendelea kusisitiza wazazi wasiwaachie walimu majukumu yote kwa sababu wao pia wanatakiwa kushiriki katika masuala yote hanayohusu elimu ikiwemo kuchangia baadhi ya michango midogo midogo ya uendeshaji wa shule.

Naye mmoja wa wanafunzi ambaye amehitimu darasa la saba katika shule hiyo ya Zegereni akisoma risala kwa niaba ya wenzake ameiomba serikali kuwasaidia kupata uzio katika shule hiyo.



Na. Asia Singano, WF – Dodoma

Wizara ya Fedha imeendesha mafunzo kwa wajumbe na wenyeviti wa Kamati za Ukaguzi wa Ndani kwa lengo la kuwajengea uwezo katika kutekeleza majukumu yao ya usimamizi, ushauri na ufuatiliaji wa utendaji wa Idara/vitengo vya ukaguzi wa ndani na mifumo ya udhibiti wa ndani katika taasisi za Serikali.

Akizungumza wakati wa kufungua Mafunzo hayo, Kaimu Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali, Wizara ya Fedha, Mhandisi Kenneth Nindie, alisema mafunzo hayo yamelenga kuwawezesha wajumbe kuelewa kwa kina wajibu wao katika kuhakikisha shughuli za ukaguzi wa ndani zinafanyika kwa ufanisi, weledi na kwa kuzingatia misingi ya maadili ya taaluma.

Alitoa rai kwa kamati hiyo kufanya kazi kwa kuzingatia maadili, weledi, uhuru na uwajibikaji ili kuimarisha mfumo wa usimamizi wa rasilimali na udhibiti wa ndani Serikalini.

‘’Nawahimiza kutekeleza majukumu yenu inavyopaswa kwa kuzingatia nidhamu pia kuhakikisha vikao vinafanyika kwa mujibu wa ratiba, wajumbe wanapata taarifa muhimu kwa wakati na wanajiandaa kabla ya vikao” Alisema Mhandisi Nindie.

Aliwataka wajumbe wa kamati hiyo kuendelea kuongeza weledi na kutumia teknolojia katika utekelezaji wa majukumu yao ili kuongeza ufanisi na matokeo chanya katika kazi za ukaguzi, kwa kuwa matumizi ya teknolojia ni miongoni mwa hatua muhimu za kuboresha utendaji wa shughuli za ukaguzi.

Alisema mabadiliko ya teknolojia yanaendelea kuathiri namna kazi za ukaguzi zinavyotekelezwa, hivyo ni muhimu kwa wakaguzi kuendana na mabadiliko hayo na kuhakikisha wanakuwa na ujuzi unaohitajika katika mazingira ya sasa ya kazi.

Awali, akimkaribisha Kaimu Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali, Wizara ya Fedha, Mhandisi Kenneth Nindie, Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali Msaidizi, Idara ya Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali, Wizara ya Fedha, Bw. Paison Mwamnyasi, aliwataka washiriki wa mafunzo hayo kuyazingatia kwa umakini ili kufikia lengo lililokusudiwa la mafunzo hayo.

‘’Mafunzo haya yana umuhimu sana kwenye utendaji wetu hivyo ni muhimu kuyazingatia ili kuleta matokeo chanya yaliyolengwa na Wizara’’ alisema Bw. Mwamnyasi.

Naye Mwezeshaji wa mafunzo hayo ambaye pia ni Mkaguzi wa Ndani Mwandamizi kutoka Idara ya Mkaguzi Mkuu wa Ndani wa Serikali, Wizara ya Fedha, Bw. Andrew Nicholaus, alieleza kuwa Kamati ya Ukaguzi ina jukumu muhimu la kusaidia mamlaka inayoteua katika kutekeleza wajibu wake wa usimamizi, huku ikitakiwa kubaki huru katika kutoa ushauri na uangalizi.

Mafunzo hayo yanayoendelea kufanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS), ni sehemu ya utekelezaji wa dhamira ya Wizara ya Fedha, ya kuimarisha mifumo ya ukaguzi wa ndani na Kamati za Ukaguzi wa ndani kama sehemu ya juhudi za kuongeza uwazi, uwajibikaji na matumizi sahihi ya rasilimali za Serikali.Na. Asia Singano, WF – Dodoma

Wizara ya Fedha imeendesha mafunzo kwa wajumbe na wenyeviti wa Kamati za Ukaguzi wa Ndani kwa lengo la kuwajengea uwezo katika kutekeleza majukumu yao ya usimamizi, ushauri na ufuatiliaji wa utendaji wa Idara/vitengo vya ukaguzi wa ndani na mifumo ya udhibiti wa ndani katika taasisi za Serikali.

Akizungumza wakati wa kufungua Mafunzo hayo, Kaimu Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali, Wizara ya Fedha, Mhandisi Kenneth Nindie, alisema mafunzo hayo yamelenga kuwawezesha wajumbe kuelewa kwa kina wajibu wao katika kuhakikisha shughuli za ukaguzi wa ndani zinafanyika kwa ufanisi, weledi na kwa kuzingatia misingi ya maadili ya taaluma.

Alitoa rai kwa kamati hiyo kufanya kazi kwa kuzingatia maadili, weledi, uhuru na uwajibikaji ili kuimarisha mfumo wa usimamizi wa rasilimali na udhibiti wa ndani Serikalini.

‘’Nawahimiza kutekeleza majukumu yenu inavyopaswa kwa kuzingatia nidhamu pia kuhakikisha vikao vinafanyika kwa mujibu wa ratiba, wajumbe wanapata taarifa muhimu kwa wakati na wanajiandaa kabla ya vikao” Alisema Mhandisi Nindie.

Aliwataka wajumbe wa kamati hiyo kuendelea kuongeza weledi na kutumia teknolojia katika utekelezaji wa majukumu yao ili kuongeza ufanisi na matokeo chanya katika kazi za ukaguzi, kwa kuwa matumizi ya teknolojia ni miongoni mwa hatua muhimu za kuboresha utendaji wa shughuli za ukaguzi.

Alisema mabadiliko ya teknolojia yanaendelea kuathiri namna kazi za ukaguzi zinavyotekelezwa, hivyo ni muhimu kwa wakaguzi kuendana na mabadiliko hayo na kuhakikisha wanakuwa na ujuzi unaohitajika katika mazingira ya sasa ya kazi.

Awali, akimkaribisha Kaimu Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali, Wizara ya Fedha, Mhandisi Kenneth Nindie, Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali Msaidizi, Idara ya Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali, Wizara ya Fedha, Bw. Paison Mwamnyasi, aliwataka washiriki wa mafunzo hayo kuyazingatia kwa umakini ili kufikia lengo lililokusudiwa la mafunzo hayo.

‘’Mafunzo haya yana umuhimu sana kwenye utendaji wetu hivyo ni muhimu kuyazingatia ili kuleta matokeo chanya yaliyolengwa na Wizara’’ alisema Bw. Mwamnyasi.

Naye Mwezeshaji wa mafunzo hayo ambaye pia ni Mkaguzi wa Ndani Mwandamizi kutoka Idara ya Mkaguzi Mkuu wa Ndani wa Serikali, Wizara ya Fedha, Bw. Andrew Nicholaus, alieleza kuwa Kamati ya Ukaguzi ina jukumu muhimu la kusaidia mamlaka inayoteua katika kutekeleza wajibu wake wa usimamizi, huku ikitakiwa kubaki huru katika kutoa ushauri na uangalizi.

Mafunzo hayo yanayoendelea kufanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS), ni sehemu ya utekelezaji wa dhamira ya Wizara ya Fedha, ya kuimarisha mifumo ya ukaguzi wa ndani na Kamati za Ukaguzi wa ndani kama sehemu ya juhudi za kuongeza uwazi, uwajibikaji na matumizi sahihi ya rasilimali za Serikali.




Kaimu Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali, Wizara ya Fedha, Mhandisi Kenneth Nindie, akizungumza wakati wa kufungua Mafunzo kwa Wajumbe na Wenyeviti wa Kamati za Ukaguzi wa Ndani, kwa lengo la kuwajengea uwezo katika kutekeleza majukumu yao ya usimamizi, ushauri na ufuatiliaji wa utendaji wa Idara/Vitengo vya ukaguzi wa ndani na mifumo ya udhibiti wa ndani katika taasisi za Serikali, yanayoendelea katika Ukumbi wa Mikutano wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS), jijini Dodoma.


Kaimu Mkaguzi Mkuu wa Ndani wa Serikali, Wizara ya Fedha, Mhandisi Kenneth Nindie (kulia), akiteta jambo na Mkaguzi Mkuu wa Ndani wa Serikali Msaidizi, Idara ya Mkaguzi Mkuu wa Ndani wa Serikali, Wizara ya Fedha, Bw. Paison Mwamnyasi baada ya kufungua Mafunzo kwa Wajumbe na Wenyeviti wa Kamati za Ukaguzi wa Ndani wa Serikali, yanayoendelea katika Ukumbi wa Mikutano wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS), jijini Dodoma.


Mkaguzi wa Ndani Mwandamizi kutoka Idara ya Mkaguzi Mkuu wa Ndani wa Serikali, Wizara ya Fedha, Bw. Andrew Nicholaus, akitoa wasilisho kuhusu masuala muhimu ya Ukaguzi wa Ndani ikiwemo maadili ya ukaguzi, wakati wa Mafunzo kwa Wajumbe na Wenyeviti wa Kamati za Ukaguzi wa Ndani, yanayoendelea katika Ukumbi wa Mikutano wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS), jijini Dodoma.


Kaimu Mkaguzi Mkuu wa Ndani wa Serikali, Wizara ya Fedha, Mhandisi Kenneth Nindie (wa pili kulia), akijadiliana jambo na Mkaguzi Mkuu wa Ndani wa Serikali Msaidizi, Idara ya Mkaguzi Mkuu wa Ndani wa Serikali, Wizara ya Fedha, Bw. Paison Mwamnyasi (wa kwanza kushoto), pamoja na Wakaguzi wengine kutoka Idara ya Mkaguzi wa Ndani wa Serikali, Wizara ya Fedha, nje ya kikao cha Mafunzo kwa Wajumbe na Wenyeviti wa Kamati za Ukaguzi wa Ndani, yanayoendelea katika Ukumbi wa Mikutano wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS), jijini Dodoma.


Kaimu Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali, Wizara ya Fedha, Mhandisi Kenneth Nindie (katikati waliyoketi), akiwa katika picha ya pamoja na Mkaguzi Mkuu wa Ndani wa Serikali Msaidizi, Idara ya Mkaguzi Mkuu wa Ndani wa Serikali, Wizara ya Fedha, Bw. Paison Mwamnyasi (wapili kushoto), pamoja na Wajumbe na Wenyeviti wa Kamati za Ukaguzi wa Ndani wa Serikali, baada ya kufungua mafunzo kwa Kamati hiyo yanayoendelea katika Ukumbi wa Mikutano wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS), jijini Dodoma.

(Picha na Kitengo Cha Mawasiliano Serikalini, WF - Dodoma)
Na HABIBA MBARUKU, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju ametoa rai kwa wadau wanaoshughulikia Mashauri ya Kodi, Biashara, Mabenki, Ardhi, Uwekezaji na Ushindani wa Kibiashara kuchukua tahadhari na hatua madhubuti za kukabiliana na mvua za El nino kufuatia taarifa iliyotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) juu ya uwepo wa mvua hizo kuanzia mwezi Oktoba mwaka huu.

Mhe. Masaju ametoa ushauri huo tarehe 16 Septemba, 2026 alipokuwa akifunga Mkutano wa nne wa Wadau kuhusu Tathmini ya Utekelezaji wa Mkakati wa Kushughulikia Mashauri ya Kodi, Biashara, Mabenki, Ardhi, Uwekezaji na Ushindani wa Kibiashara uliofanyika kwenye ukumbi wa mikutano, Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Akizungumza na Wadau hao, Mhe. Masaju amesema kuwa, Serikali inachukua hatua za kujikinga na kukabiliana na janga hilo hivyo, na wao wanapaswa kuchukua tahadhari kila mmoja na kutazama ni kwa namna gani wanaweza kuendeleza shughuli ikiwa mvua hizo zitakuwepo, pia kila mmoja kwa imani yake kumuomba Mwenyezi Mungu bila kusubiri kuambiwa na viongozi wa dini na pasipo kuringia kiburi cha uzima.

“Wadau wa haki mmejiandaa vipi, TLS mmeshaandaa namna gani ya kuendelea kusikiliza mashauri haya, wakati pengine njia barabarani hazifikiki, kwenye ‘Law fame’ zenu mna vyumba vya kutosha, Ofisi ya Taifa ya Mashtaka, Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali na wadau wengine humu tumejiandaa namna gani, hayo ndiyo ya kutafakari, sisi wenyewe kwenye sekta hii tuchukue hatua namna gani tutaendeleza shughuli zetu kama hilo janga litakuwepo, lakini pia na kumuomba Mwenyezi Mungu atukinge alitupilie mbali hilo janga, tusiwe na kiburi cha uzima, tuone kama Mungu yupo, maji yana nguvu Ghorofa hazisaidii kitu chochote,” amesema Jaji Mkuu.

Aidha, amesisitiza juu ya maombi huku akirejea Kitabu cha Zaburi 103, kama muongozo katika maombi ambayo itawawezesha wadau kuomba kwa yale ambayo yapo nje ya uwezo wao kuyadhibiti, basi Mwenyezi Mungu kwa rehema na fadhili zake aingilie kati na kuliepusha Taifa na janga hilo kwa sababu hakuna ambaye ana kinga ya uhakika ya kujiweka salama pindi janga hilo litakapotokea.

“Sisi wengine hatuna kinga ya kutofikiwa na hayo majanga ya elnino kama yatakuwepo, yapo mengine yapo nje ya uwezo wetu, na mimi naamini uwepo wa Mwenyezi Mungu, kila mmoja hapa hakuna ambaye anakinga ya kutokufa kwa majanga, kila mmoja achukue tahadhari na kumuomba Mwenyezi Mungu, lazima tuwe tayari kumuomba kwa rehema, neema na fadhili zake kwa mujibu wa Zaburi ya 103 ambayo tunaishi kwayo, anaweza kuingilia kati akatunusuru kwakuwa hata uwezo wetu wa kujikinga na hayo majanga ni mdogo,” ameongeza Mhe. Masaju.

Katika hatua nyingine, Jaji Mkuu amebainisha changamoto ambazo zinasababisha ucheleweshaji wa usikilizaji wa mashauri ya kiuchumi, ambazo amezitaja kuwa ni changamoto zinazotokana na Mahakama yenyewe, changamoto za kisheria na changamoto zinazotokana na wadau.

Amesema kuwa, changamoto zinazotokana na Mahakama yenyewe ni hasa zile za kisheria, ambazo zinaambatana na mfumo wa kitaasisi na kushauri kuwa wadau waendelee kubaini changamoto hizo na kuzijadili kwa pamoja ili kuzipatia ufumbuzi pale ambapo mhusika amekwama kuzitatua.

Amezitaja changamoto hizo kuwa ni ufunguaji wa mashauri kwa lengo la kuchelewesha ulipaji wa madeni, ambapo watu hufungua mashauri mahakamani ili wasiwajibike kulipa deni na kuongeza kuwa, kukiwa na riba rafiki na upatikanaji wa elimu hususan elimu ya mikopo na masuala ya bima watu watapata uelewa wa kutosha na kufahamu wajibu wao na namna gani wanawajibika.

Kadhalika, ameitaja changamoto nyingine kuwa, ni matumizi ya mbinu za kiufundi ili kuchelewesha usikilizaji na uamuzi wa mashauri, hali ya kuwa Katiba imetoa muongozo wa kutofungwa kupita kiasi na masharti ya kiufundi yanayoweza kukwamisha haki kutendeka akirejelea Ibara ya 107A(2)(e) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, (1977).

“Matumizi ya mbinu za kiufundi ili kuchelewesha usikilizaji na uamuzi wa mashauri hizi (legal technicalities), wakati Katiba imetoa mwongozo kwamba tusifungwe kupita kiasi na masharti ya kiufundi yanayoweza kukwamisha haki kutendeka, hilo sharti limetajwa kwenye Ibara ya 107A(2)(e) haki inapaswa itendeke, tunapojiendekeza kwenye hizi hili tunaahirisha tu mgogoro hatuwezi kutatua mgogoro,” ameongeza Mhe. Masaju.

Pamoja na hayo, Jaji Mkuu amesema kwamba, wadau wanapaswa kuendelea kudhibiti hatua zinazochelewesha usikilizaji wa migogoro kwa kurahisisha matumizi ya notisi ya siku 90, kwa kuangalia wanaohusika kumfanya yule anayepewa notisi kutaka kushtakiwa, awajibike kuchukua hatua ambazo ni za kutatua na ikiwa ni hatua za usuluhishi wajadiliane ili kurahisisha usikilizaji wa migogoro na kuwataka wanaohusika na kuchakata notisi wawajibike ili kumaliza migogoro mapema ipasavyo.

“Wale wanaohusika na kuchakata hizo notisi zinazotolewa na watu wanaotaka kuishtaki Serikali na Taasisi zake, wawajibike kushughulikia hiyo changamoto inayopelekea watake kushtakiwa, kwa namna hiyo migogoro mingi itaisha,” amesema Mhe. Masaju.

Katika hatua nyingine, Jaji Mkuu ameongeza kuwa, uwajibikaji ni moja ya nyenzo inayotajwa katika Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050 pia ni sharti la kikatiba kama Ibara ya 25 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inavyosisitiza juu ya uwajibikaji, kujituma na kuzingatia nidhamu ili kufikia malengo yaliyowekwa, hivyo ameipongeza Tume ya Taifa ya Mipango kwa mkakati wanaouweka ili kuleta uwajibikaji.

“Uwajibikaji ni sharti la kikatiba, kitu kikishawekwa kwenye sheria tunawajibika kukitekeleza kwa sababu huwa kuna adhabu usipokitekeleza kwa hiyo Ibara ya 25 ya Katiba inatusisitiza juu ya uwajibikaji lakini pia inasisitiza juu ya kujituma na inasisitiza juu ya kuzingatia nidhamu ya kazi ili kufikia malengo tuliyojiwekea,” amesema Mhe. Masaju.

Aidha, katika matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), amesema Mahakama imepiga hatua kubwa kwa kuweka mifumo mbalimbali ya matumizi ya TEHAMA huku mifumo mingine ikiendelezwa na kuwasisitiza wadau hao kuendelea kuimarisha matumizi ya TEHAMA kama yanavyosisitizwa katika Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050. Ametaja manufaa ya kutumia TEHAMA katika utendaji kuwa ni pamoja na kupunguza matumizi ya karatasi ili kuimarisha mwenendo wa mashauri, kupunguza muda na gharama za kiutawala, kuongeza uwazi na uwajibikaji, kuwezesha upatikanaji wa taarifa mapema ipasavyo na kutoa takwimu zinazoweza kusaidia katika kupanga na kupima utendaji wa Mahakama.

Akihitimisha hotuba yake, Jaji Mkuu amemtaka kila mdau wa haki kujitathmini, kubaini changamoto zake za kiuwezo, kiutendaji na kimaadili na kuzifanyia kazi ili kwa pamoja kufikia matarajio ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050.





Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akizungumza wakati ya kufunga Mkutano wa nne wa Wadau kuhusu Tathmini ya Utekelezaji wa Mkakati wa Kushughulikia Mashauri ya Kodi, Biashara, Mabenki, Ardhi, Uwekezaji na Ushindani wa Kibiashara tarehe 16 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano, Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.



Sehemu ya Viongozi wa Mahakama na Wadau wengine wakiwa katika Mkutano wa nne wa Wadau kuhusu Tathmini ya Utekelezaji wa Mkakati wa Kushughulikia Mashauri ya Kodi, Biashara, Mabenki, Ardhi, Uwekezaji na Ushindani wa Kibiashara tarehe 16 Septemba, 2026 uliofanyika kwenye ukumbi wa mikutano, Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.




Wajumbe wa Mkutano wakifuatilia hotuba ya Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (hayupo katika picha) alipokuwa akifunga Mkutano wa nne wa Wadau kuhusu Tathmini ya Utekelezaji wa Mkakati wa Kushughulikia Mashauri ya Kodi, Biashara, Mabenki, Ardhi, Uwekezaji na Ushindani wa Kibiashara tarehe 16 Septemba, 2026 uliofanyika kwenye ukumbi wa mikutano, Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi (kulia) akichangia jambo wakati wa Mkutano wa nne wa Wadau kuhusu Tathmini ya Utekelezaji wa Mkakati wa Kushughulikia Mashauri ya Kodi, Biashara, Mabenki, Ardhi, Uwekezaji na Ushindani wa Kibiashara tarehe 16 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano, Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.(Picha na Mary Gwera, Mahakama)

Top News