Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amewataka wananchi wa Kizimkazi na maeneo ya Kusini Unguja kutunza na kudumisha miradi ya maendeleo, ikiwemo maji, afya na barabara, ili iendelee kutoa huduma bora kwa wananchi.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, tarehe 14 Agosti 2026, katika kilele cha Tamasha la Kizimkazi 2026 kilichofanyika Uwanja wa Mwehe, Makunduchi, Mkoa wa Kusini Unguja.

Amesema miradi hiyo ni muhimu katika kuboresha maisha ya wananchi na kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii, hivyo wananchi wanapaswa kushirikiana na Serikali katika kuitunza na kuhakikisha inatumika kwa malengo yaliyokusudiwa.

Aidha, Rais Dkt. Mwinyi amesema Tamasha la Kizimkazi limeendelea kuwa jukwaa muhimu la kutangaza utalii, utamaduni na fursa za uwekezaji, kukuza vipaji, pamoja na kuwaunganisha wafanyabiashara na wajasiriamali na masoko mapya.

Ameipongeza Kamati ya Maandalizi kwa kuendelea kulikuza tamasha hilo na kusisitiza kuwa Serikali itaendelea kuunga mkono matukio yanayochangia kukuza utalii, utamaduni, biashara, ajira na kipato kwa wananchi.

Tamasha la Kizimkazi 2026 lilifunguliwa tarehe 12 Agosti 2026 na Rais Dkt. Mwinyi na kuhitimishwa leo, tarehe 14 Agosti 2026, na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika Uwanja wa Mwehe, Makunduchi, Mkoa wa Kusini Unguja. 














NA: MWANDISHI WETU, ZANZIBAR 

Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake wa Chama Cha Mapinduzi (UWT) Taifa, Mary Chatanda, ameungana na viongozi na wananchi katika Tamasha la Kizimkazi katika mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar.

Akizungumzia tamasha hilo,  Agosti 13, 2026, Chatanda amesema, linasaidia kukuza upendo, mshikamano na maendeleo miongoni mwa viongozi na wananchi, hivyo linapaswa kuendelezwa. 

"Tamasha la Kizimkazi linawaleta watu pamoja kutoka maeneo tofauti nchini, hili ni jambo kubwa sana, tunaongea na kubadilishana mawazo. Pia, miradi ya maendeleo kama ya elimu, afya, maji inazinduliwa katika kutatua kero za wananchi," amesema Chatanda

Aidha, amepongeza suala la utamaduni kuenziwa katika tamasha hilo, kwani utamaduni una umuhimu mkubwa katika kuliheshimisha taifa na kukuza maendeleo.

"Upekee mwingine wa tamasha hili ni kuenzi utamaduni wetu yaani mavazi, vyakula, ngoma za asili, lugha yetu ya Kiswahili, tukumbuke kuwa utamaduni unaibua fursa za kiuchumi katika kuongeza kasi ya maendeleo," amesisitiza.

Katika tamasha hilo, Chatanda ameshiriki uzinduzi na ukaguzi wa mradi wa Makaazi wa Amani (Amani Residency) na upandaji miti katika Kituo cha Afya Kizimkazi.

Viongozi mbalimbali wakiwemo Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, Dk. Hussein Mwinyi, mawaziri, wabunge, viongozi wa Chama, serikali na wananchi mbalimbali wameshiriki tamasha hilo ambalo linagusa nyanja zote za kijamii, kiuchumi na kisiasa katika kukuza maendeleo nchini.











Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, akizungumza alipotembelea banda la Kampuni ya Mawasiliano Yas katika Maonesho ya Tamasha la Kizimkazi, Mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar, Agosti 12, 2026. Yas ni miongoni mwa wadau muhimu wa Uchumi wa Buluu na maendeleo ya utalii Zanzibar, kupitia uwekezaji wake katika miundombinu ya mawasiliano na huduma za kidijitali zinazochangia kuimarisha muunganisho na ukuaji wa sekta ya utalii visiwani humo.




 

Serikali imevitaka vyama vya wafanyakazi nchini, ikiwemo Chama cha Walimu Tanzania (CWT), kutumia meza ya majadiliano (Social Dialogue) kutatua kero za wafanyakazi badala ya  migongano isiyo na tija inayodhoofisha mshikamano na kushusha morali ya kazi.

Rai hiyo imetolewa na Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi,Ajira na Mahusiano Mheshimiwa Dr. Evaline Munisi wakati akifungua rasmi mafunzo ya siku mbili kwa watumishi wa Makao Makuu na Makatibu wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT) wa Mikoa na Wilaya kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi hiyo Deus Sangu leo Agosti 13, 2026 mjini Morogoro.

Amesema kuwa Vyama vya Wafanyakazi havikuundwa kwa ajili ya kusigana na Waajiri, bali viliundwa kama jukwaa la kisheria la kukaa meza moja na waajiri ili kujadiliana kwa hoja, ushahidi na kuheshimiana.

"Vyama vya wafanyakazi havikuundwa kwa ajili ya kusigana na waajiri, bali viliundwa kama jukwaa la kisheria la kukaa meza moja ili kupata suluhu ya pamoja. Katika miaka ya hivi karibuni tumeona kuibuka kwa makundi yanayojielekeza zaidi katika propaganda na migongano, jambo linalodhoofisha mshikamano wa walimu na kuathiri ubora wa elimu," alisema.

Akiangazia kaulimbiu ya CWT inayosema "Wajibu na Haki, Naibu Waziri amesema kuwa  mambo hayo mawili ni kama ndugu pacha wanaotembea pamoja, hivyo ni lazima walimu watimize wajibu wao wa kiutumishi kabla ya kudai haki zao.

Amesema ni wajibu wa chama hicho kutetea maslahi ya walimu kama mishahara, upandaji vyeo na malimbikizo, lakini pia ni wajibu wao kuwasimamia walimu wafundishe kwa juhudi na nidhamu.

"Mwalimu asiyetimiza wajibu wake, anayetoroka kazini au anayekiuka maadili anakosa halali ya kimaadili ya kudai haki zake na anakiharibia chama sifa njema. Utendaji bora darasani ndio unaoipa CWT nguvu ya kusimama mbele ya Serikali kudai haki," alisema.

Ameongeza kuwa ulimwengu wa leo unaendeshwa na mifumo ya kidijitali na sheria, hivyo mtazamo wa zamani wa kuendesha vyama kwa mazoea na mihemko hauna nafasi tena, Serikali inatarajia kuona mabadiliko makubwa katika kasi ya kutatua kero za walimu na uadilifu wa matumizi ya fedha baada ya mafunzo hayo.

Katika hatua nyingine, Naibu Waziri amesema kuwa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan inaendelea kufanya uwekezaji mkubwa katika sekta ya elimu kwa kujenga miundombinu na kuajiri walimu wapya ili kupunguza mzigo wa kazi.

Aidha Serikali itaendelea kuweka mazingira bora ya kazi na kushirikiana na CWT ili kulinda amani na utulivu mahali pa kazi. Mafunzo hayo ya siku mbili yamejumuisha washiriki takriban 240 yakilenga kuwajengea uwezo katika sheria za kazi, taratibu za Tume ya Utumishi wa Walimu (TSC), na utendaji wa Bodi ya Kitaaluma ya Walimu.

Aikizungumza awali mwakilishi wa Msajili wa Vyama vya Wafanyakazi na Waajiri Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Ajira na Mahusiano Mussa Msami amesema kuwa kitengo cah Msajili wa Vyama vya Wafanyakazi na Waajiri milango iko wazi kwa ushauri ushirikiano wakati wote. 






Na Belinda Joseph-Dodoma.

Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Mkoa wa Dodoma limefanya kikao kikao kazi na Maafisa wa Jeshi la Polisi ngazi ya kata, wilaya na Mkoa wa Dodoma, kwa lengo la kuimarisha ushirikiano katika ulinzi wa miundombinu ya umeme na kutoa elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa kulinda miundombinu hiyo.

Akizungumza katika kikao hicho, Kaimu Meneja wa TANESCO Mkoa wa Dodoma, Mhandisi Kurwa Mangara, amesema ushirikishwaji wa vyombo vya ulinzi ni muhimu kutokana na nafasi ya umeme katika maisha ya wananchi na shughuli za kiuchumi.

Amesema hatua hiyo imechukuliwa kutokana na changamoto za uhujumu na uharibifu wa miundombinu ya uzalishaji, usafirishaji na usambazaji wa umeme, ikiwemo wizi wa vyuma na bolti pamoja na uvamizi wa maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya njia za kusafirisha umeme.

Mangara ameeleza kuwa baadhi ya maeneo hayo yamekuwa yakitumika kwa shughuli za kilimo na uchimbaji wa mchanga na kokoto, hali inayoweza kusababisha mmomonyoko wa udongo na kuhatarisha nguzo pamoja na miundombinu mingine ya umeme.

Aidha, ametaja changamoto ya kuibiwa nyaya zinazotumika kulinda transfoma na kuchomwa kwa nguzo za umeme wakati wa uandaaji wa mashamba vitendo ambavyo vinaweza kusababisha kukatika kwa umeme, hasara kwa TANESCO na usumbufu kwa wananchi.

Ametoa wito kwa wananchi kutambua thamani ya miundombinu ya umeme na kuacha vitendo vinavyoweza kuhatarisha upatikanaji wa nishati hiyo, akisisitiza kuwa ulinzi wa miundombinu ya umeme ni jukumu la pamoja kwa TANESCO, vyombo vya ulinzi na usalama pamoja na wananchi.

Kwa upande wake, Kaimu Afisa wa Jeshi la  Polisi  ASP Regina Mtana, amewashukuru TANESCO kwa kutoa elimu hiyo na kuahidi kuwa Jeshi la Polisi litaendelea kushirikiana na shirika hilo katika kuimarisha ulinzi wa miundombinu ya umeme na kuchukua hatua dhidi ya vitendo vinavyoweza kuhatarisha usalama na upatikanaji wa nishati hiyo.





Na Mwandishi Wetu, Dar

Waziri wa Ujenzi, Mhe. Abdallah Ulega (Mb.) amefurahishwa na Huduma zinazotolewa na Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA) hususan matumizi ya Moduli ya kupokea na kushughulukia malalamiko na rufaa katika mfumo wa NeST. 

Waziri Ulega ameipongeza PPAA alipotembelea banda la Mamlaka hiyo pembezoni mwa Mkutano wa Mashauriano na Wadau wa Sekta ya Ujenzi kwa Mwaka 2026 unaofanyika tarehe 13 – 14, Agosti, 2026 Jijini Dar es Salaam. 

PPAA imeshiriki maaonesho hayo kwa lengo la kutoa elimu juu ya huduma mbalimbali inazozitoa kwa wadau wa ununuzi wa umma hususan matumizi ya Moduli ya kupokea na kushughulukia malalamiko na rufaa katika mfumo wa NeST. 

Hongereni kwa kazi nzuri ya kutoa elimu kwa wadau wenu hasa wakandarasi walioshiriki katika mkutano wa leo, endeleeni kufanya kazi hii nzuri ili kutimiza azma ya Serikali ya kuwasogezea wananchi huduma kwa karibu zaidi,” amesema Mhe. Ulega 
Kwa Upande wake Mkuu wa Sehemu ya Huduma za Sheria PPAA, Bi. Agnes Sayi ambaye alimwakilisha Katibu Mtendaji wa PPAA, Bw. James Sando alimweleza Waziri Ulega kuwa kuanza kwa matumizi ya Moduli ya kupokea malalamiko na rufaa katika mfumo wa NeST kumechangia kuongeza uwazi, uwajibikaji na ufanisi kwenye mnyororo wa ununuzi na ugavi. 

“Mhe. Waziri matumizi ya moduli katika mnyororo wa ununuzi na ugavi yamechangia kutoa maamuzi kwa haki na wakati na kuwezesha miradi ya Serikali kutekelezwa kwa wakati,” amesema Bi. Sayi

Pamoja na mambo mengine, Bi. Sayi amemweleza Mhe. Ulega kuwa  kwa sasa PPAA inatoa huduma ya Mkutano kwa njia ya Mtandao “Video Conference” ambapo hutumika kusikiliza mashauri ya wazabuni walioshindwa kufika katika Ofisi za Mamlaka ya Rufani kwa ajili ya kusikiliza rufaa zilizowasilishwa.

“Huduma ya ‘video conference’ inatoa fursa ya kuwasikiliza wazabuni walioshindwa kufika PPAA na hivyo kuiwezesha Mamlaka ya Rufani kutekeleza jukumu lake la msingi la utatuzi wa migogoro itokanayo na michakato ya ununuzi wa Umma kwa haki na wakati,” ameongeza Bi. Sayi

Awali akifungua Mkutano wa Mashauriano na Wadau wa Sekta ya Ujenzi kwa Mwaka 2026 unaoendelea Jijini Dar es Salaam, Waziri Ulega amewataka Wakandarasi wazawa na wakandarasi wote nchini kwa ujumla kuhakikisha kuwa wanatekeleza miradi wanayoipata kwa weledi na ufanisi.

Aidha, Waziri Ulega ameongeza Serikali imeandaa mikakati ya kuwasaidia Wakandarasi wazawa na Washauri Elekezi ili waweze kunufaika kupitia miradi inayotolewa nchini na kuwataka watendaji wa Wizara ya Ujenzi kutoa ushirikiano na kuhakikisha wanatatua changamoto zinazowakwamisha wakandarasi wa ndani kupata miradi.

Mkutano wa Mashauriano na Wadau wa Sekta ya Ujenzi, umeongozwa na Kaulimbiu, “Dira 2025: Fursaa na Wajibu wa Makandarasi katika ujenzi wa Miundombinu Endelevu”


 

NA DENIS MLOWE IRINGA

MKUU wa Mkoa wa Iringa, Kheri James, amezindua Kliniki ya Watumishi wa Umma inayolenga kusikiliza na kutatua kero zinazowakabili watumishi na wastaafu katika Mkoa wa Iringa, akisisitiza kuwa utatuzi wa changamoto za watumishi ni msingi wa kuboresha huduma zinazotolewa kwa wananchi.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa kliniki hiyo uliofanyika katika viwanja vya Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Kheri amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuboresha mazingira ya kazi kwa watumishi wa umma kupitia maboresho ya mishahara, upandishaji wa madaraja, ajira mpya na kuimarisha mifumo ya usimamizi wa rasilimali watu.

Alisema pamoja na hatua hizo, bado zipo changamoto zinazowakabili baadhi ya watumishi na wastaafu, ikiwemo malimbikizo ya mishahara, madai ya likizo, uhamisho, matibabu, kupandishwa madaraja, mafao ya wastaafu pamoja na fidia kwa watumishi wanaoumia kazini.

“Lengo la kliniki hii siyo kutafuta makosa ya watu, bali kutafuta suluhisho la madai, manung’uniko na changamoto za watumishi na wastaafu ili wafanye kazi wakiwa na utulivu wa akili, motisha na imani kuwa haki zao zinapatikana pale inapostahili,” alisema Kheri.

Amesema kliniki hiyo ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kuwafikia watumishi walipo badala ya kuwalazimisha kutumia muda na fedha kusafiri kwenda maeneo mbalimbali kufuatilia changamoto ambazo zinaweza kutatuliwa ndani ya mkoa.

Kheri alisema kuwa mpango huo ni muhimu hasa kwa watumishi wanaotoa huduma za moja kwa moja kwa wananchi, wakiwemo madaktari, walimu na watumishi wengine, ambao wanapokuwa na changamoto zisizotatuliwa wanaweza kushindwa kufanya kazi kwa ufanisi unaotarajiwa.

“Tunataka watumishi wetu wafanye kazi wakiwa na furaha na utulivu tunatatua changamoto za watu wetu ili nao wakaweze kutatua changamoto za wananchi wenzao,” amesema.

Ameongeza kuwa kliniki hiyo itasaidia pia kupunguza muda na gharama ambazo watumishi wamekuwa wakitumia kufuatilia masuala yao katika taasisi za Serikali zilizopo nje ya mkoa

“Yawezekana mwalimu ana jambo linaloweza kushughulikiwa na Ofisi ya Utumishi ya Mkoa au Wilaya, lakini akalazimika kusafiri hadi TAMISEMI au Utumishi hivyo hii kliniki inarahisisha jambo hilo kushughulikiwa hapa hapa Iringa,” amesema.

Kheri pia amewataka viongozi na wataalamu wanaoshiriki katika kliniki hiyo kutoa huduma kwa weledi, uadilifu na heshima, kusikiliza kila mtumishi na mstaafu bila ubaguzi na kutoa majibu yanayozingatia sheria, kanuni na miongozo ya Serikali.

Amesisitiza kuwa pale ambapo suala haliwezi kutatuliwa papo hapo, mtumishi apewe mrejesho wa hatua zitakazochukuliwa pamoja na muda wa utekelezaji, huku akitaka hakuna changamoto inayopuuzwa au kuachwa bila kufuatiliwa.

Aidha amesema ustawi wa watumishi unapaswa kwenda sambamba na ustawi wa wananchi, akieleza kuwa Serikali inapoboresha mishahara, madaraja na mazingira ya kazi, watumishi nao wanapaswa kulipa kwa kutoa huduma bora kwa wananchi.

“Serikali imeshughulika na madaraja, mishahara na maeneo mazuri ya kufanya kazi sisi jitihada hiyo inayofanywa na Serikali lazima tuitafsiri kwa huduma bora kwa wananchi. Ustawi wa watumishi uende sambamba na ustawi wa wananchi,” amesema Kheri.
Kliniki hiyo inafanyika kuanzia Agosti 13 hadi 20, 2026, katika halmashauri zote tano za Mkoa wa Iringa, ambapo watumishi na wastaafu watapata fursa ya kuwasilisha changamoto zao na kupata ufumbuzi au maelekezo ya namna ya kuzifanyia kazi.

Kwa upande wake, Nuru Sobela, ambaye ni mratibu wa Kliniki ya Watumishi wa Umma Mkoa wa Iringa na Katibu Tawala Msaidizi anayeshughulikia masuala ya Utumishi na Usimamizi wa Rasilimali Watu, amesema kliniki hiyo imeandaliwa kwa ajili ya kusikiliza kero na changamoto mbalimbali zinazowakabili watumishi wa umma.

Amesema katika kliniki hiyo yameandaliwa madawati mbalimbali, ikiwemo dawati la mfumo, mishahara, masuala ya watumishi wanaoumia kazini pamoja na dawati maalum kwa ajili ya wastaafu.

Ameeleza kuwa dawati la wastaafu linafanya kazi kwa kushirikiana na PSSSF ili kuhakikisha changamoto za wastaafu zinapatiwa ufumbuzi.
Mbali na masuala ya utumishi, amesema taasisi mbalimbali zimeungana na zoezi hilo kutoa huduma kwa watumishi, zikiwemo NHIF, NIDA na taasisi za benki.

Nuru amewataka watumishi wote wa umma katika Mkoa wa Iringa kutumia fursa hiyo kufikisha changamoto zao ili zipatiwe ufumbuzi kwa wakati.

Amesema baada ya uzinduzi wa kliniki hiyo katika makao makuu ya mkoa, zoezi litaendelea katika maeneo mengine, ambapo tarehe 17 na 18 Agosti litafanyika Wilaya ya Kilolo, huku tarehe 19 na 20 Agosti likifanyika Wilaya ya Mufindi.

Amesema dhamira ya Serikali ni kuhakikisha mtumishi anapata mazingira rafiki ya kuwasilisha hoja zake, kufuatilia haki zake na kupata majibu bila kutumia gharama kubwa au muda mwingi wa kuacha kituo chake cha kazi.





Na Janeth Raphael - MichuziTv

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda, amezitaka Kamati za Ushauri wa Stadi (TACs) za Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) kuhakikisha mafunzo yanayotolewa yanaendana na mahitaji halisi ya soko la ajira, teknolojia na mabadiliko ya sekta mbalimbali. Prof. Mkenda amesema mafunzo ya ufundi stadi hayapaswi kuishia katika utoaji wa vyeti, bali yanapaswa kumwandaa mhitimu kuwa na ujuzi, umahiri, ubunifu, nidhamu ya kazi na uwezo wa kutumia teknolojia katika kufanya kazi na kujiajiri.

Akizungumza leo Agosti 13, 2026, jijini Dodoma wakati wa uzinduzi wa Kamati hizo, Prof. Mkenda amesema TACs zinapaswa kuwa “macho na masikio” ya VETA kwa kufuatilia mabadiliko ya teknolojia, uzalishaji na mahitaji ya waajiri katika maeneo ya kazi. Amesisitiza kuwa kamati hizo zisibaki kuwa za mikutano pekee, bali ziwe za matokeo kwa kutoa ushauri wa wakati kuhusu maboresho ya mitaala, kuanzishwa kwa stadi mpya na kuondolewa kwa teknolojia zilizopitwa na wakati.

Waziri Mkenda amesema ushauri wa TACs ni muhimu katika kuhakikisha vijana wanaohitimu wanakuwa na ujuzi unaohitajika na waajiri, huku VETA ikipata fursa ya kuanzisha programu mpya katika sekta zenye fursa za ajira na kujiajiri, ikiwemo TEHAMA, utalii, ukarimu, sanaa, ujenzi, nishati, kilimo na uzalishaji. Amesema waajiri wanapaswa kuwa sehemu ya mfumo wa mafunzo kwa kueleza mahitaji yao ya ujuzi, vifaa, teknolojia na viwango vya utendaji vinavyohitajika.

Akihusisha hatua hiyo na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Prof. Mkenda amesema Tanzania haiwezi kuwa na uchumi imara, jumuishi na shindani bila kuwa na nguvu kazi yenye ujuzi. Amesema elimu na mafunzo ya ufundi stadi ni nyenzo muhimu katika kujenga viwanda vya kisasa, uchumi wa kidijitali na uwezo wa Taifa kuzalisha bidhaa na huduma kwa kutumia maarifa, teknolojia na ubunifu wa ndani.

Aidha, Prof. Mkenda amesema kuanzishwa kwa TACs ni sehemu ya utekelezaji wa Sera ya Elimu na Mafunzo ya Mwaka 2014, Toleo la 2023, inayosisitiza elimu inayokidhi mahitaji ya maendeleo ya Taifa na soko la ajira. Ameeleza pia kuwa Serikali imeendelea kuimarisha ushirikiano kati ya taasisi za elimu na sekta ya viwanda kupitia Mpango wa Kitaifa wa Ushirikiano kati ya Taasisi za Elimu na Sekta ya Viwanda katika Ukuzaji wa Ujuzi na Uwezeshaji wa Ajira, uliozinduliwa Februari 9, 2026, jijini Dar es Salaam.

Prof. Mkenda amewataka wajumbe wa TACs kutekeleza majukumu yao kwa uadilifu, weledi, ubunifu, uwajibikaji na uzalendo, huku wakiwa mabalozi wa VETA katika sekta zao na kuhamasisha waajiri kushirikiana na taasisi hiyo katika kuandaa mitaala, kutoa mafunzo kwa vitendo, kuboresha teknolojia na kuandaa nguvu kazi yenye ujuzi unaohitajika. Amesisitiza kuwa utekelezaji wa Dira 2050 hautategemea mipango na nyaraka pekee, bali Watanzania wenye maarifa, ujuzi, ubunifu, nidhamu na uwezo wa kutumia teknolojia.



RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ametembelea banda la Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) katika Maonesho yanayoambatana na Tamasha la 10 la Kizimkazi, Mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar.

Katika ziara hiyo, Mhe. Rais Samia amepongeza PSSSF kwa kushiriki katika maonesho hayo na kutoa huduma pamoja na elimu kwa wanachama na wananchi wanaotembelea banda la Mfuko.

Mhe. Rais Samia alipokelewa na Meneja wa PSSSF Ofisi ya Zanzibar, Bi. Mariam Saleh, ambaye alimueleza kuhusu huduma zinazotolewa na Mfuko, pamoja na namna wanachama na wananchi wanavyonufaika na huduma hizo kupitia banda hilo.

Mhe. Rais Samia ameupongeza Mfuko kwa utoaji wa huduma na kusisitiza umuhimu wa kusikiliza na kushughulikia kwa wakati changamoto zinazowasilishwa na wananchi na wanachama.

“Nawapongeza sana kwa huduma nzuri. Kama kuna malalamiko, yakusanyeni na muyafanyie kazi,” ameagiza Mhe. Rais Samia.

Ushiriki wa PSSSF katika Tamasha la Kizimkazi unalenga kuendelea kuwafikia wanachama na wananchi kwa kuwapatia elimu kuhusu hifadhi ya jamii, huduma zinazotolewa na Mfuko pamoja na kuwawezesha kupata ufafanuzi wa masuala mbalimbali yanayohusu mafao na huduma za PSSSF.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Siuluhu Hassan, akizungumza alipotembelea banda la Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) kwenye Maonesho ya Tamasha la Kizimkazi Mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar Agosti 12, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (kulia), akimsikiliza Meneja wa Ofisi ya Zanzibar ya Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) Bi. Mariam Saleh, alipotembelea banda la Mfuko huo kwenye Maonesho ya Tamasha la Kizimkazi 2026 (Kizimkazi Festival 2026) Mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar Agosti 12, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (kushoto), akimsikiliza Meneja wa Ofisi ya Zanzibar ya Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) Bi. Mariam Saleh, alipotembelea banda la Mfuko huo kwenye Maonesho ya Tamasha la Kizimkazi 2026 (Kizimkazi Festival 2026) Mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar Agosti 12, 2026.


 

Naibu Waziri wa Nishati, Mhe.Salome Makamba,akipata maelezo mara baada ya kutembelea  banda la Mamlaka ya Udhibiti Huduma za Nishati na Maji (EWURA) katika Maonesho ya Kizimkazi yanayoendelea katika Viwanja vya Dimbani, Kizimkazi, Zanzibar.

Na Mwandishi Wetu

Naibu Waziri wa Nishati, Mheshimiwa Salome Makamba, amehimiza umma kupata taarifa sahihi kuhusu hali ya sekta ndogo ya umeme nchini, huku akitoa wito kwa Mamlaka ya Udhibiti Huduma za Nishati na Maji (EWURA) kuendelea kutoa elimu na taarifa kwa wananchi kuhusu jitihada mbalimbali zinazofanywa na Serikali katika kuboresha huduma za umeme.

Mhe. Makamba ametoa wito huo leo, tarehe 13 Agosti 2026, alipotembelea banda la EWURA katika Maonesho ya Kizimkazi yanayoendelea katika Viwanja vya Dimbani, Kizimkazi, Zanzibar.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, amesema ni muhimu wananchi kupata taarifa sahihi kuhusu kuongezeka kwa uzalishaji na upatikanaji wa umeme nchini na hivyo kukidhi mahitaji tuliyonayo.

“Gharama ya umeme nchini Tanzania ni nafuu ikilinganishwa na nchi jirani, na Serikali inaendelea na juhudi za kuboresha na kuimarisha miundombinu ya umeme ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma hiyo kwa uhakika, hatua itakayochochea maendeleo ya kiuchumi nchini,” aliongeza.

Katika banda la EWURA, Mhe. Makamba alifahamishwa Mamlaka imetumia fursa ya Maonesho hayo kutoa elimu kuhusu masuala mbalimbali ya udhibiti ikiwemo mikataba ya huduma kwa wateja, matumizi sahihi na salama ya huduma za bidhaa za gesi ya mitungi, gesi asilia, umeme na maji, fursa za uwekezaji katika sekta na mengineyo.

Naibu Waziri wa Nishati, Mhe.Salome Makamba,akisaini kitabu  mara baada ya kutembelea  banda la Mamlaka ya Udhibiti Huduma za Nishati na Maji (EWURA) katika Maonesho ya Kizimkazi yanayoendelea katika Viwanja vya Dimbani, Kizimkazi, Zanzibar.

 

Naibu Waziri wa Nishati, Mhe.Salome Makamba,akipata maelezo mara baada ya kutembelea  banda la Mamlaka ya Udhibiti Huduma za Nishati na Maji (EWURA) katika Maonesho ya Kizimkazi yanayoendelea katika Viwanja vya Dimbani, Kizimkazi, Zanzibar.


Top News