Na Janeth Raphael -MichuziTv -Bungeni Dodoma

SERIKALI imesema inaendelea kuchukua hatua mbalimbali kuhakikisha taaluma na kazi ya udereva nchini zinapata staha, hadhi na heshima inayolingana na kada nyingine katika utumishi wa umma.

Kauli hiyo imetolewa na Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Regina Qwaray, wakati akijibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi (Mlalo) lililouliza kuhusu mkakati wa Serikali wa kuinua hadhi ya taaluma ya udereva.

Akijibu swali hilo, Naibu Waziri Qwaray amesema Serikali imeendelea kuchukua hatua kadhaa zikiwemo kuboresha Muundo wa Maendeleo ya Utumishi wa Kada ya Udereva, ili kuwawezesha watumishi wa kada hiyo kupata fursa za maendeleo ya kiutumishi.

Amesema Serikali pia inaendelea kuboresha mafunzo ya kitaaluma pamoja na viwango vya elimu kwa madereva, hatua inayolenga kuongeza weledi, ufanisi na uwezo wa watumishi hao katika kutekeleza majukumu yao.

Kwa mujibu wa Naibu Waziri huyo, Serikali pia imeendelea kuimarisha motisha na maslahi ya kada ya udereva, kwa kuzingatia mazingira ya kazi na mahitaji ya utendaji, ili kuhakikisha madereva wanatekeleza majukumu yao katika mazingira yanayostahili.

Hatua hizo, amesema, ni sehemu ya juhudi za Serikali kuhakikisha kada ya udereva inatambuliwa na kuthaminiwa kama taaluma yenye mchango muhimu katika utendaji wa Serikali na utoaji wa huduma kwa wananchi.



 


Taasisi za LALJI FOUNDATION na BARAKA  FOUNDATION  kwa kushirikiana na  VISION 4 ALL EYE CENTER  imeendesha Kambi ya Matibabu ya Macho Bure katika Halmashauri ya Mji wa Korogwe, Mkoa wa Tanga, kwa lengo la kuwasaidia wananchi kupata huduma za uchunguzi, matibabu na upasuaji wa macho bila gharama.

Kambi hiyo iliyofanyika kwa muda wa siku tatu imewafikia jumla ya wananchi 3,259, ambao walihudhuria na kupata huduma mbalimbali za afya ya macho.

Akizungumza baada ya kutamatika kwa kambi hiyo mwenyekiti wa LALJI FOUNDATION Imtiaz Lalji amesema kwa siku zote tatu, jumla ya wagonjwa 333 walifanyiwa  upasuaji wa macho, Kati yao, 291 walibainika kuwa na tatizo la mtoto wa jicho (cataract), huku 39 wakiwa na matatizo madogo ya macho yaliyohitaji huduma za upasuaji.

Aidha, jumla ya wananchi 1,723 walipewa dawa kulingana na mahitaji yao ya kiafya, huku wananchi 1,706  wakipatiwa miwani ya kusomea (reading glasses).

Imtiaz Lalji, amesema taasisi hiyo itaendelea kushirikiana na Serikali kuwasaidia Watanzania kupata matibabu ya macho bila malipo, kutokana na changamoto ya magonjwa ya macho ambayo imeendelea kuwaathiri wananchi wengi.

“Takwimu zilizopatikana katika kambi hiyo zinaonesha ukubwa wa changamoto ya magonjwa ya macho katika jamii, akibainisha kuwa wananchi wa maeneo ya vijijini ni miongoni mwa wanaokumbwa zaidi na changamoto ya upatikanaji wa huduma za macho kwa wakati" ameongeza

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Korogwe, Bi. Zahara Msangi, ameishukuru LALJI FOUNDATION na Baraka FOUNDATION  kwa kuguswa na changamoto zinazowakabili wananchi na kuamua kufikisha huduma za matibabu ya macho katika Halmashauri hiyo.

Amesema huduma hiyo imekuwa na umuhimu mkubwa kwa wananchi, hususan wale ambao wamepata fursa ya kufanyiwa uchunguzi, kupata dawa, miwani pamoja na upasuaji bila kulipia gharama.

Naye Mratibu wa Huduma za Macho Mkoa wa Tanga, Dkt. Husein Abassy, amesema kuletwa kwa huduma hiyo mkoani Tanga ni hatua muhimu inayolenga kuwafikia wananchi wenye uhitaji, hususan wale ambao wanakabiliwa na changamoto ya kupata huduma za macho kwa wakati.

Nao baadhi ya wananchi walionufaika na kambi hiyo wameeleza namna huduma hizo zilivyowasaidia kupata matibabu ambayo huenda wasingeweza kuyapata kwa urahisi kutokana na gharama.

Wameishukuru LALJI FOUNDATION kwa huduma hiyo na kutoa wito kwa taasisi nyingine, mashirika na wadau mbalimbali kuendelea kujitokeza na kushirikiana na Serikali katika kuboresha afya na ustawi wa wananchi.

Huduma hiyo ya matibabu ya macho bila malipo ni sehemu ya juhudi za LALJI FOUNDATION  katika kusaidia jamii na kupunguza changamoto ya upatikanaji wa huduma za afya kwa wananchi.

 Taasisi hiyo imeahidi kuendelea kushirikiana na Serikali na wadau wengine katika kuwafikia wananchi wenye uhitaji katika maeneo mbalimbali nchini.






Na Mwandishi wetu, Simanjiro

MKUU wa Wilaya ya Simanjiro Mkoani Manyara, Fakii Raphael Lulandala ameingilia kati mgogoro wa ardhi kwa kuagiza waliovamia eneo la shule ya serikali ya Saniniu Laizer ya kijiji cha Naepo Kata ya Naisinyai kusitisha ujenzi wake.

DC Lulandala ameagiza waliovamia eneo hilo kusitisha shughuli za ujenzi na ndani ya siku 14 tafsiri ya mipaka ifanywe na wataalam wa ardhi na kuweka alama ya mipaka eneo la shule hiyo ya Saniniu Laizer.

Hata hivyo, Lulandala ameagiza uhakiki wa eneo la ekari 48 la mipaka ya shule hiyo ufanyike upya kwa usimamizi wa wataalamu wa ardhi na apewe taarifa baada ya siku saba.

Amewaagiza polisi na taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa (Takukuru) kuwahoji ofisa mtendaji wa kata hiyo Valentine Tesha, Mwenyekiti wa kijiji hicho Elias Abraham na aliyejenga nyumba eneo hilo Stephen Mollel.

"Haiwezekani mtendaji wa kata Tesha na Mwenyekiti wa kijiji, nyumba ijengwe na kupauliwa ninyi mnaona tuu bila kuchukua hatua, polisi na Takukuru wahojini hawa viongozi kwa nini waliruhusu," amesema DC Lulandala.

Mchimbaji maarufu wa madini ya Tanzanite, bilionea Saniniu Laizer ambaye alijenga shule hiyo na kuikabidhi serikali amepongeza hatua iliyochukuliwa na DC Lulandala.

Diwani wa kata ya Naisinyai, Taiko Kurian amesema eneo hilo lilikuwa mali ya kijiji na likatengwa ekari 48 kwa ajili ya ujenzi wa shule hiyo ya awali na msingi ya serikali.

Mmoja kati ya watu wanaodaiwa kujenga nyumba eneo hilo Stephen John Mollel amekiri kupewa barua mbili tofauti za kusimamisha ujenzi wake ila akaendelea kujenga.

Na. Philipo Hassan - Dodoma

Kamishna wa Uhifadhi wa Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA), Massana Mwishawa leo Agosti 31, 2026 amekielekeza Kitengo cha Mahusiano ya Jamii kuongeza wigo wa utoaji wa elimu ya uhifadhi kwa wananchi hususan jamii zinazozunguka Hifadhi za Taifa ili kuwawezesha wananchi hao kushiriki katika shughuli za uhifadhi na maendeleo.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa Kikao Kazi cha Mwaka cha Kitengo cha Mahusiano ya Jamii cha TANAPA, kinachofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Ofisi Kiunganishi TANAPA jijini Dodoma, Kamishna Mwishawa alieleza kuwa  elimu ya uhifadhi ni muhimu katika kujenga uelewa na mahusiano mazuri kati ya Shirika na jamii.

“Ninasisitiza umuhimu wa kuendelea kutoa elimu ya uhifadhi kwa jamii ili kuwaelimisha wananchi namna ya kukabiliana na changamoto ya wanyamapori wakali na waharibifu, kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi, kutunza na kuhifadhi vyanzo vya maji, kujikita kwenye shughuli za uzalishaji mali kupitia utalii pamoja na kusimamia na kufuatilia utekelezaji wa miradi ya ujirani mwema kwa kuhamasisha ushiriki wa vikundi mbalimbali vya kijamii,” alisema Kamishna Mwishawa.

Sambamba na hilo, Kamishna Mwishawa alieleza kuwa Kitengo cha Mahusiano ya Jamii kinapaswa kuwa kiunganishi kati ya TANAPA na jamii kutokana na kuwa na mahusiano ya moja kwa moja na wananchi, hivyo kina nafasi muhimu katika kuimarisha shughuli za uhifadhi, ulinzi na usalama wa watalii.

Kwa upande wake, Afisa Uhifadhi Mkuu na Kaimu Mkuu wa Sehemu ya Uhifadhi, Glory Summay alibainisha kuwa  kikao hicho ni muhimu katika kutathmini utekelezaji wa majukumu ya Kitengo cha Mahusiano ya Jamii, kubadilishana uzoefu uliopatikana, kubaini changamoto na kuweka mikakati ya kuimarisha ushirikiano kati ya TANAPA na jamii zinazozunguka hifadhi.

“Kikao hiki kitatupa fursa ya kutathmini tulipofikia, kujifunza kutokana na uzoefu wetu na kuweka mikakati madhubuti ya kuimarisha mahusiano na jamii kwa manufaa ya kuboresha maliasili katika Hifadhi za Taifa”, alieleza Mhifadhi Summay.

Kitengo cha Mahusiano ya Jamii kinatumia kikao hicho kuweka mikakati ya kuimarisha utendaji wa Kitengo, kuongeza maarifa na ujuzi wa utendaji kazi, hususan katika matumizi ya mfumo wa ukusanyaji taarifa, pamoja na kujengeana uelewa wa pamoja kuhusu mbinu bora za ushirikishwaji wa jamii kwa ajili ya kuboresha mahusiano na kuongeza ushiriki wa wananchi katika shughuli za uhifadhi.

Dhana ya ushirikishwaji wa jamii kwenye shughuli za uhifadhi ni jambo muhimu kwani Wananchi ndiyo msingi wa uhifadhi wa maliasili zilizopo. Ni dhahiri kuwa, uhifadhi hauwezi kufanikiwa kama jamii siyo sehemu ya uhifadhi huo.









 Fikiria unatua katika nchi mpya na intaneti yako tayari inafanya kazi kabla hata hujatoka uwanja wa ndege. Hakuna haja ya kutafuta Wi-Fi. Hakuna kununua SIM card ya ndani. Wala kulipa gharama kubwa za kutumia huduma ya intaneti ukiwa nje ya nchi (roaming).

Programu mpya ya Kwetu eSIM inamwezesha mtu yeyote kununua kifurushi cha intaneti kwa ajili ya safari kabla ya kusafiri na kukiwasha ndani ya chini ya dakika moja. Hakuna SIM card ya kawaida ya kubadilisha, hakuna kifaa kidogo cha kufungulia sehemu ya SIM card cha kubeba, wala foleni katika maduka ya huduma za simu uwanja wa ndege. Unachotakiwa kufanya ni kuchagua unakokwenda, kufanya malipo, kuskani QR code au kuingiza msimbo wa usajili, na kuanza kutumia intaneti katika nchi zaidi ya 190. Kwetu eSIM inakubali malipo kwa kadi pamoja na huduma za fedha kwa njia ya simu, ikiwemo Airtel Money na Mix, kupitia DPO na pochi ya fedha ndani ya programu. Kwetu eSIM inafanya kazi kwenye simu za iPhone na Android na inatumia lugha mbalimbali, hivyo kurahisisha huduma kwa wasafiri kutoka maeneo mbalimbali duniani. Hakuna SIM card. Hakuna usumbufu wa roaming. Unatua tu na kuunganishwa. Programu ya Kwetu eSIM sasa inapatikana kwenye Apple App Store na Google Play, huku vifurushi vya intaneti kwa ajili ya safari vikiweza pia kununuliwa kupitia kwetuesim.com. Kwa maelezo zaidi, tembelea kwetuesim.com au https://kwetuesim.com/sw/

KUTAZAMA VIDEO BONYEZA HAPA

Dar es Salaam, Agosti 31, 2026 Serikali ya Somalia imeendelea kuchukua hatua za kuimarisha mageuzi ya utumishi wa umma kwa kujipanga kuanzisha Chuo cha Taifa cha Utumishi wa Umma huku ikilenga kutumia uzoefu wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) katika uendeshaji wa taasisi ya mafunzo ya watumishi wa umma.Hayo yameelezwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Shirikizo ya Somalia, Mhe. Hirsi Jama Ganni ulipotembelea Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) akiongoza ujumbe wa serikali hiyo ikiwa ni sehemu ya ziara rasmi ya siku nne nchini Tanzania iliyolenga kujifunza uzoefu wa Tanzania katika mageuzi ya sekta ya umma, mabadiliko ya kidijitali na maboresho ya mifumo ya Serikali.


Mhe. Ganni amesema Somalia imeweka mageuzi ya utawala wa umma kuwa moja ya vipaumbele vya kitaifa na kwamba mafanikio ya Serikali yanategemea kuwa na watumishi wenye ujuzi na uwezo wa kubadilisha sera na mipango kuwa matokeo halisi kwa wananchi.

“Somalia inapanga kuanzisha Chuo cha Taifa cha Utumishi wa Umma kitakachokuwa na jukumu la kutoa mafunzo kwa watumishi wa Serikali, kuanzia mafunzo ya awali kwa watumishi wapya hadi mafunzo kwa viongozi waandamizi. amesema Mhe. Ganni”

Mhe. Ganni ameongeza kuwa Tanzania imejenga mfumo ambao Somalia kwa sasa inalenga kuuanzisha, hivyo ziara hiyo imekuwa muhimu kwao katika kujifunza namna TPSC inavyoandaliwa, jinsi mitaala inavyotengenezwa na kusasishwa, pamoja na namna taasisi inavyoweza kuendelea kuwa na umuhimu katika kukabiliana na mabadiliko ya vipaumbele vya Serikali.

“Tuna matumaini ziara hii itakuwa mwanzo wa ushirikiano wa muda mrefu katika maeneo ya uandaaji wa mitaala, kubadilishana wakufunzi na uzoefu, ujenzi wa taasisi pamoja na matumizi ya majukwaa ya kidijitali katika mafunzo,” amesema Mhe. Ganni
Akizungumzia ziara hiyo, Mkuu wa Chuo na Mtendaji Mkuu wa TPSC, Dkt. Ernest Mabonesho, amesema ujumbe huo umetembelea Tanzania kwa lengo la kujifunza namna utumishi wa umma unavyoendeshwa nchini, huku ziara ya TPSC ikiwa na msisitizo wa kujifunza kuhusu uanzishwaji na uendeshaji wa chuo cha utumishi wa umma.

Dkt. Mabonesho amesema Somalia ilikuwa na chuo cha utumishi wa umma hapo awali, lakini taasisi hiyo ilishindwa kuendelea kufanya kazi kutokana na changamoto zilizotokana na vita, hivyo sasa nchi hiyo inapanga kuanzisha upya taasisi hiyo kwa kujifunza kutoka nchi mbalimbali ikiwemo Tanzania.

Ameeleza kuwa mafunzo ya utumishi wa umma ni muhimu kwa kuwaunganisha wataalamu kutoka kada mbalimbali wanaohudumu katika Serikali, wakiwemo madaktari, wahandisi na wahasibu, ili wote wawe na uelewa wa maadili, wajibu na namna bora ya kuwahudumia wananchi kwa heshima na staha.

Katika hatua nyingine, Dkt. Mabonesho amesema ziara hiyo imekuwa na manufaa pia kwa TPSC kutokana na uzoefu na maswali yanayotolewa na wageni hao, ambayo yanaweza kusaidia Chuo kutafakari na kuboresha baadhi ya maeneo ya utendaji.

Amesema miongoni mwa maeneo yaliyovutia mjadala ni utaratibu wa baadhi ya nchi kuwapatia watumishi wa umma mafunzo na mitihani kabla ya kuingia rasmi katika utumishi wa umma, akieleza kuwa suala hilo linaweza kusaidia kuwaandaa watumishi kabla ya kuanza kutekeleza majukumu yao.








 


SHIRIKA la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC) limetoa wito kwa sekta binafsi kuongeza uwekezaji katika bandari kavu, maeneo ya kuhifadhi makontena na miundombinu ya maegesho ya malori ili kukabiliana na ongezeko la mizigo inayopita katika Bandari ya Dar es Salaam.

TASAC imesema ongezeko la idadi ya makontena yanayohudumiwa katika Bandari ya Dar es Salaam linatokana na kuimarika kwa mazingira ya uwekezaji pamoja na maboresho yaliyofanyika katika huduma za bandari.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mkuu wa TASAC, Mohamed Salum, amesema kuongezeka kwa shughuli za bandari kumeongeza mahitaji ya malori na maeneo ya kuhifadhi makontena.

Amesema maboresho hayo yameongeza ufanisi wa huduma za bandari, ikiwemo kupunguza muda wa 
kuhudumia meli na upakuaji wa makontena.

Kwa mujibu wa TASAC, mwezi Julai pekee Bandari ya Dar es Salaam ilihudumia takribani makontena 137,000, hali inayoonyesha kuongezeka kwa shughuli za biashara kupitia bandari hiyo.

TASAC imeeleza kuwa ongezeko hilo linahitaji maandalizi zaidi katika miundombinu ya usafirishaji na uhifadhi wa makontena, hususan kuongeza idadi ya malori na maeneo ya bandari kavu.

“Wenye bandari kavu wanapaswa kuongeza maeneo kwa ajili ya malori. Hii ni fursa na siyo laana,” imeelezwa.

Shirika hilo pia limewataka wamiliki wa bandari kavu kupanua maeneo ya maegesho ya malori na kuongeza uwezo wa kuhifadhi makontena ili kusaidia kupunguza msongamano katika maeneo ya bandari.

TASAC imesisitiza kuwa ongezeko la makontena ni fursa ya kiuchumi inayopaswa kuungwa mkono na sekta binafsi kupitia uwekezaji katika bandari kavu, malori na maeneo ya kuhifadhi makasha.

Aidha, TASAC imeonya dhidi ya taarifa na kauli zinazoweza kutoa taswira hasi kuhusu shughuli za Bandari ya Dar es Salaam, ikisema baadhi ya kauli zinaweza kupotosha mafanikio yaliyopatikana katika kuboresha huduma za bandari.

Kwa upande mwingine, TASAC imeeleza kuwa kwa kushirikiana na waendeshaji wa bandari, ikiwemo DP World, uwezo wa kuhudumia meli umeongezeka, huku baadhi ya meli kubwa zikihudumiwa ndani ya muda mfupi.

Meneja wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA), Abed Gallus, amesema mamlaka hiyo inaendelea kujiandaa kukabiliana na ongezeko la mizigo kwa kuboresha uwezo wa kuhifadhi na kuhamisha makontena kutoka eneo moja kwenda jingine ndani ya bandari.

TASAC imeeleza kuwa meli yenye takribani makontena 3,000 inaweza kuhudumiwa ndani ya siku moja, hatua inayosaidia kupunguza muda wa meli kukaa bandarini na kuongeza ufanisi wa usafirishaji wa mizigo.

Katika kipindi cha miaka miwili iliyopita, shughuli za Bandari ya Dar es Salaam zimeendelea kukua, huku ongezeko la mizigo likiongeza mahitaji ya miundombinu ya usafirishaji na uhifadhi.

Katika upande wa bandari kavu, Bandari Kavu ya Kwala ina uwezo wa kuhudumia takribani makontena 300,000 kwa mwaka, huku taarifa zikitaja kuwa uwezo wake wa kuhifadhi na kuhudumia makontena unahitaji kuendana na ongezeko la mizigo inayopita katika Bandari ya Dar es Salaam.

Aidha, takribani makontena 1,350 yaliyopo Bandari Kavu ya Kwala yanahitaji kuondolewa ili kuongeza nafasi ya kuhifadhi na kuwezesha bandari hiyo kuendelea kuhudumia mizigo inayoongezek


-AWATAKA WATUMISHI KUACHA KUFANYA KAZI KWA MAZOEA

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Deogratius Ndejembi, amewataka watumishi wa Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira kuongeza bidii, uwajibikaji na kuachana na utendaji wa kazi kwa mazoea ili kuhakikisha majukumu ya Serikali yanatekelezwa kwa ufanisi na kwa wakati.

Makamu wa Rais ametoa wito huo leo, alipofanya ziara yake ya kwanza katika Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), iliyopo Mtumba, jijini Dodoma, ambako alipokelewa na wafanyakazi pamoja na Menejimenti ya Wizara hiyo.

Amesisitiza umuhimu wa watumishi kubadili mitazamo na namna ya kufanya kazi, akitaka kila mmoja kuwa mbunifu na kuweka mipango inayolenga kuleta matokeo yanayoonekana kwa wananchi na Taifa kwa ujumla.

Makamu wa Rais amewasihi watumishi kutumia nafasi zao kutoa huduma yenye thamani kwa watanzania na kutambua dhamana waliyonayo katika kuwahudumia wananchi. Pia amewataka kubadili mitazamo na namna ya kufikiri, kuwa wabunifu na kuhakikisha mipango inayowekwa inaleta tija na matokeo chanya katika shughuli mbalimbali zinazotekelezwa kwa maslahi mapana ya Taifa.

Halikadhalika, amewataka kuongeza jitihada katika kudumisha Muungano kwa kuwa na mipango endelevu inayolenga kutatua changamoto mbalimbali pamoja na kutoa elimu ya fursa zilizopo katika Muungano.

Amewasihi Viongozi na Watumishi wa Wizara hiyo, kuwa na mipango endelevu katika utekelezaji wa ajenda ya ulinzi na uhifadhi wa mazingira kwa kutumia vema kampeni za upandaji miti, usafi wa majiji na miji kwa kuweka nyenzo zitakazosaidia kufanya hali hiyo kuwa endelevu. Vile vile amesisitiza umuhimu wa kuwa na Mpango maalum utakao saidia wananchi kuhama katika shughuli za kila siku zinazoharibu mazingira.

Awali, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhandisi Hamad Masauni, amempongeza Makamu wa Rais kwa kuaminiwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika nafasi hiyo na kumhakikishia ushirikiano katika kutekeleza majukumu mbalimbali yanayohusu Ofisi ya Makamu wa Rais.

Akiwasilisha taarifa kuhusu shughuli zinazotekelezwa na idara mbalimbali zilizo chini ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Katibu Mkuu, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Dkt. Richard Muyungi, amesema wizara hiyo ina Idara nne, Vitengo nane na Taasisi mbili zinazotekeleza majukumu mbalimbali, ikiwemo utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 katika masuala ya Muungano na Mazingira.






Jeshi la Polisi Mkoa wa Geita linamshikilia Jackline Peter, mkazi wa Mji Mdogo wa Katoro, Wilaya na Mkoa wa Geita, kwa tuhuma za kumshambulia kwa fimbo Rahel Jumanne baada ya kumtilia shaka kumwibia fedha.

Akitoa taarifa hiyo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita amesema tukio hilo la kikatili lilitokea tarehe 26 Agosti 2026, saa 5.00 asubuhi nyumbani kwa mtuhumiwa Katoro.

Inadaiwa mtuhumiwa aligundua amepoteza fedha kiasi cha Shilingi 60,000/= zilizokuwa kwenye pochi chumbani kwake. Baada ya hapo alimtilia shaka Rahel Jumanne aliyekuwa amemtembelea kwake.

Kamanda amesema baada ya fedha hizo kudaiwa kupotea, mtuhumiwa alimkamata mwathirika na kuanza kumshambulia kwa fimbo.

Katika tukio hilo, mfanyakazi wa kazi za ndani wa mtuhumiwa alielekezwa kurekodi vitendo hivyo kwa kutumia simu ya mtuhumiwa. Baadaye mtuhumiwa mwenyewe alisambaza picha mjongeo hiyo kwenye mitandao ya kijamii.

Baada ya Jeshi la Polisi kubaini tukio hilo kwenye mitandao ya kijamii, lilifanya ufuatiliaji wa haraka na kufanikiwa kubaini eneo la tukio, kumtambua mtuhumiwa na kumkamata. Kwa sasa anaendelea kuhojiwa.

Kamanda amesema uchunguzi wa tukio hilo unaendelea na mara utakapokamilika mtuhumiwa atafikishwa katika mamlaka husika za kisheria kwa hatua zaidi.

Aidha ametoa wito kwa baadhi ya wananchi kuacha tabia ya kujichukulia sheria mkononi.

"Tuhuma za uhalifu hazimruhusu mtu kutoa adhabu mwenyewe. Mtu anatakiwa kutoa taarifa kwa mamlaka za kisheria ili hatua zichukuliwe," amesisitiza.



JESHI la Polisi mkoa wa Kilimanjaro linamshikilia Mwanafunzi wa kidato cha tatu katika shule ya sekondari Kisarika wilayani Moshi, Nelson Mkenda (17), kwa tuhuma za kumjeruhi mwanafunzi mwenzake aitwaye Vicent Mmary, (17) wa shule ya Sekondari Kisarika, kidato cha tatu kwa kitu chenye ncha kali kifuani na kusababisha kifo chake.

Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo, Kamanda wa Polisi mkoa wa Kilimanjaro, SACP Saimon Maigwa alisema kuwa, tukio hilo limetokea Agosti 28 mwaka huu majira ya saa tisa na robo alasiri huko katika shule ya Sekondari Kisarika, kitongoji cha Manushi, kijiji cha Ongomauru, Kata ya Uru Kaskazini, Wilaya ya Moshi.

Alisema kuwa, ulitokea ugonvi baina yao baada ya Marehemu kumtuhumu Mtuhumiwa kuiba vitu mbalimbali kwenye mabweni ya shule hiyo.

Mwanafunzi huyo alifariki dunia akiwa njiani kuelekea hospitali ya Rufaa ya Mkoa ya Mawenzi kwa matibabu.

Uchunguzi wa kina unaendelea ili kukamilisha taratibu za kisheria na kumfikisha mtuhumiwa Mahakamani.

Na Janeth Raphael - MichuziTv


Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kimeendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ya kuimarisha uzalishaji wa mapato ya ndani kwa kuanzisha kampuni ya uwekezaji itakayoratibu na kusimamia vitengo mbalimbali vya uzalishaji visivyo vya kitaaluma, hatua inayolenga kuongeza ufanisi, tija na uwezo wa Chuo kujiendesha kibiashara.

Akizungumza na vyombo vya habari kuhusu mafanikio ya SUA katika kipindi cha Awamu ya Sita, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu hicho, Prof. Raphael Chibunda, amesema SUA kupitia kampuni yake ya uwekezaji ya SUA Income Generation & Services Ltd, inaendelea kutekeleza mikakati madhubuti ya kutumia rasilimali zake katika shughuli zenye uwezo wa kuzalisha mapato na kuchochea maendeleo ya Chuo.

Amesema katika kutekeleza mkakati huo, ukarabati wa majengo ya Kiwanda cha Uchapishaji (Printing Unit) pamoja na Kitengo cha Maziwa (Dairy Unit) umekamilika, huku baadhi ya mitambo ya uchapishaji ikiwa tayari imefungwa na kuwekwa katika hali ya kuanza uzalishaji.

Prof. Chibunda amesema SUA pia inaendelea kutumia mitambo ya Feed Mill & Silos kwa ajili ya uzalishaji wa chakula cha mifugo, kuku na samaki, hatua ambayo pamoja na kusaidia mahitaji ya uzalishaji wa Chuo, inalenga pia kuongeza mapato kupitia shughuli za kibiashara.

Katika kuimarisha uwekezaji wa muda mrefu, amesema SUA imeanza kutumia rasilimali zake za misitu katika fursa za uchumi wa kijani, ambapo Msitu wa Ifinga wenye ukubwa wa hekta 10,000, uliopo Wilaya ya Madaba mkoani Ruvuma, unalengwa kutumika katika biashara ya kimataifa ya hewa ukaa (Carbon Trading).

Amesema tayari hekta 1,500 za msitu huo zimepandwa miti ya biashara, hatua inayoweka msingi wa Chuo kushiriki katika soko la kimataifa la hewa ukaa huku kikihakikisha matumizi endelevu ya rasilimali za misitu.

Aidha, amesema SUA imeendelea kuwekeza katika kilimo cha mazao yenye fursa za kibiashara, ambapo katika Shamba la Biashara lililopo Kampasi ya Solomon Mahlangu, jumla ya ekari 200 za mkonge zimepandwa na ekari 100 za mwanzo tayari zimefikia hatua ya kuanza kuvunwa kwa ajili ya uzalishaji wa nyuzi za katani.

Prof. Chibunda amesema katika kuimarisha usimamizi wa shughuli hizo, mwezi Mei 2026 Baraza la Chuo liliunda Bodi ya Usimamizi na kumteua Meneja wa Mpito wa SUA Income Generation & Services Ltd, kwa ajili ya kuanza utekelezaji wa shughuli za kampuni hiyo.

Amesema kampuni hiyo inatarajiwa kuchukua na kusimamia vitengo vyote vya uzalishaji ambavyo si vya kitaaluma lakini vina uwezo mkubwa wa kuzalisha mapato kwa Chuo, ikiwemo Shamba la Biashara la Kampasi ya Solomon Mahlangu pamoja na vitengo vyake vya maziwa, nguruwe, malisho, shamba na uzalishaji wa chakula cha mifugo.

Vitengo vingine vinavyolengwa kuingia katika uwekezaji huo ni pamoja na Kiwanda cha Samani cha Vuyisile (Vuyisile Mini Furniture Factory) kilichopo Kampasi ya Solomon Mahlangu na SUA Printing Press kilichopo Kampasi ya Edward Moringe.

Kwa upande mwingine, amesema maghala mawili yaliyopo Kampasi ya Solomon Mahlangu yako katika mpango wa ukarabati ili yaweze kutumika kuanzisha kiwanda kidogo cha kuchakata matunda na kuzalisha bidhaa mbalimbali zikiwemo sharubati, maji ya kunywa pamoja na tomato sauce.

Mbali na shughuli hizo, Prof. Chibunda amesema SUA imeendelea kuwekeza katika maeneo mengine ya kimkakati kwa ajili ya kuimarisha shughuli za kitaaluma na kuongeza mapato ya ndani, ikiwa ni pamoja na uzalishaji wa chakula cha samaki na mifugo pamoja na uzalishaji wa matofali kwa ajili ya mafunzo na biashara.

Amesema Chuo pia kinaendelea kupanda miti na kununua vifaa vya kisasa vya kukatia magogo katika eneo lake la Msitu wa Mafunzo wa Olmotonyi jijini Arusha, huku kikiboresha Shamba la Mafunzo la Mfano kwa ajili ya kutoa mafunzo ya vitendo kwa wanafunzi, wakulima na wadau wengine.

Kwa mujibu wa Prof. Chibunda, Shamba hilo pia linatumika kama chanzo cha mapato ya ndani kupitia uzalishaji na uuzaji wa miche, matunda, mbogamboga, maziwa, vifaranga vya samaki na bidhaa nyingine za kilimo. Shamba hilo lina mazao na mifugo inayowakilisha kanda mbalimbali za Tanzania, ikiwemo samaki, ng’ombe, mbuzi, kuku, kondoo, ngamia, farasi na sungura.

Aidha, SUA imeendelea kuboresha miundombinu yake katika maeneo mbalimbali, ikiwemo majengo ya Morning Sight kwa ajili ya shughuli za utalii, pamoja na majengo ya Chuo yaliyopo mjini ambayo yanalengwa kutumika katika shughuli mbalimbali za kuongeza mapato.

Katika sekta ya afya, Prof. Chibunda amesema Chuo kimeendelea kuboresha Hospitali ya SUA kwa kuongeza miundombinu ya kutolea huduma, ikiwemo ujenzi wa wodi za wagonjwa na ununuzi wa vifaa tiba, hatua inayolenga kuongeza uwezo wa hospitali hiyo kutoa huduma bora kwa jamii.

Amesema uwekezaji huo ni sehemu ya mkakati mpana wa SUA wa kutumia ipasavyo rasilimali ilizonazo, kuimarisha shughuli za kitaaluma na uzalishaji, kuongeza vyanzo vya mapato na kujenga uwezo wa Chuo kujiendesha kwa ufanisi zaidi kupitia shughuli za kibiashara na uzalishaji wa ndani.



NA MWANDISHI WETU, DODOMA

Makamu wa Rais, Deogratius Ndejembi, ameelezwa kuwa kiongozi mahiri, muadilifu na mzalendo, mwenye uwezo wa kumsaidia majukumu Rais Dk. Samia Suluhu Hassan.

Hayo yameelezwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake wa Chama Cha Mapinduzi (UWT) Taifa, Mary Chatanda, Agosti 30, 2026, ofisini kwake Dodoma, siku moja baada ya kukamilika uapisho wa kiongozi huyo, Ikulu ya Chamwino, Dodoma.

Chatanda ameeleza, Ndejembi ni kiongozi wa vitendo na katika majukumu aliyoaminiwa tangu akiwa Mkuu wa wilaya ya Kongwa, Mbunge, Naibu Waziri na Waziri kamili katika wizara mbalimbali.

"Kule Kongwa Dodoma akiwa Mkuu wa wilaya alifanya kazi nzuri na katika kilimo alisimamia kwa mafanikio makubwa kampeni yake aliyoiita ONJAKO yaani Ondoa Njaa Kongwa. Alihimiza wananchi kulima mazao yanayostahimili ukame kama mtama, mihogo, ufuta na alizeti ili kuwaepusha wananchi na kadhia ya njaa," amesema Chatanda.

Ameongeza kuwa, kampeni ya ONJAKO ilipokelewa vizuri na wakulima wa Kongwa kutokana na mwanzo kutilia mkazo zao la mahindi ambalo mara kwa mara walikuwa wakipata mazao kidogo kutokana na changamoto ya ukame wilayani humo.

Akisisitiza utendaji uliotukuka wa Ndejembi, Chatanda amesema, Wizara kadhaa alizohudumu zikiwemo Tamisemi, Vijana, Ardhi, Nishati, ameacha alama kubwa kwa kuwa mstari wa mbele kutatua changamoto za wananchi.

"Ndejembi si mtu wa kukaa ofisini kusubiri taarifa, anakwenda mwenyewe kujionea utekelezaji wa majukumu na maagizo mbalimbali. Ndiyo maana nasema, Rais Dk. Samia amepata msaidizi mchapakazi na hodari kwelikweli," ameongeza.

Katika hatua nyingine, Mwenyekiti huyo wa UWT Taifa, ametoa rai kwa wananchi kumuombea Rais Dk. Samia, Makamu wa Rais, Ndejembi na viongozi wengine ili waweze kusimamia mipango iliyopo ambayo imejikita katika kukuza ustawi na maendeleo ya wananchi.

Awali, katika uapisho huo, Rais Dk. Samia amemuasa Makamu wa Rais Mteule kuwatumikia Watanzania bila kujali tofauti zao ili kufanikisha utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2025-2030 na Dira ya Maendeleo ya miaka 25 ijayo (2050).



Na Janeth Raphael – MichuziTv, Dodoma

Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), Profesa Raphael Chibunda, ameeleza kwa kina historia ya mradi wa mafunzo na utafiti wa panya unaoendeshwa na chuo hicho kwa zaidi ya miaka 25, huku akifichua namna panya shujaa Magawa alivyoweka historia duniani kabla ya kufariki.

Prof. Chibunda amezungumza hayo leo jijini Dodoma katika Mkutano na wanahabari, ambapo amesema mradi huo umekuwa ukifanyika SUA kwa zaidi ya miaka 25, ukiwalenga panya wanaofundishwa kufanya kazi mbalimbali za utafiti na huduma za kijamii, huku akibainisha kuwa panya hao wanaotumika katika mradi huo ni wa asili ya Tanzania.

Kwa mujibu wa Prof. Chibunda, panya hao walitokana na eneo la Milima ya Uluguru mkoani Morogoro, lakini kutokana na kukua kwa mradi huo, SUA kwa sasa ina kituo maalum kinachoshughulikia uzalishaji, malezi na mafunzo ya panya hao.

Amesema mfumo wa malezi na mafunzo ya panya hao umeandaliwa kwa namna ya kipekee chuoni hapo, ambapo kuna maeneo maalum kwa ajili ya panya wanaozalishwa, wanaoanza mafunzo, wanaomaliza mafunzo pamoja na wale wanaostaafu.

“Ukimfika kwetu utakuta tuna wodi ya wazazi, tuna wanaoanza mafunzo, waliohitimu, lakini pia tuna banda la panya wastaafu. Wako pale wanapata pensheni,” amesema Prof. Chibunda.


MAGAWA ALIWEKA HISTORIA CAMBODIA

Akizungumzia panya maarufu duniani Magawa, Prof. Chibunda amesema alikuwa miongoni mwa panya waliopewa mafunzo nchini Tanzania na baadaye kupelekwa Cambodia kwa ajili ya kusaidia kutambua mabomu ya ardhini.

Amesema uamuzi wa kumpeleka Magawa nchini Cambodia ulitokana na ukweli kwamba Tanzania haikuwa na changamoto kubwa ya mabomu ya ardhini kama ilivyokuwa katika baadhi ya maeneo ya nchi hiyo ya Kusini-Mashariki mwa Asia.

Magawa alifanya kazi hiyo kwa mafanikio makubwa na hatimaye kuingia katika historia ya dunia baada ya kugundua idadi kubwa ya mabomu ya ardhini, akivunja rekodi na kuwa miongoni mwa wanyama mashuhuri zaidi waliowahi kutumika katika kazi hiyo.

Uwezo wake wa kugundua mabomu ulimfanya kupata umaarufu mkubwa kimataifa, huku akitunukiwa pia nishani ya heshima kutokana na mchango wake katika kuokoa maisha ya watu na kusaidia kuondoa mabomu hatari yaliyokuwa yamesalia ardhini.


UMRI WA PANYA NA KIFO CHA MAGAWA


Prof. Chibunda amesema panya wanaofundishwa katika mradi huo wana wastani wa maisha wa takribani miaka minane, huku miaka tisa ikiwa ni hatua ya uzee mkubwa kwa panya hao.

Ameeleza kuwa wanapofikia umri huo, huanza kudhoofika kimwili na wanaweza hata kupoteza meno, hali inayowafanya kushindwa kuendelea na shughuli zinazohitaji uwezo mkubwa wa kimwili.

Magawa naye alifikia hatua hiyo ya uzee na hatimaye kufariki dunia akiwa nchini Cambodia, baada ya kutumikia kwa mafanikio katika kazi ya kutambua mabomu ya ardhini.


SUA ILITAKA MAGAWA AREJESHWE TANZANIA

Akijibu swali kuhusu iwapo kulikuwa na mpango wa kumrejesha Magawa nchini Tanzania baada ya kufariki, Prof. Chibunda amesema mpango huo uliwahi kufikiriwa, lakini changamoto za taratibu na vibali vya usafirishaji zilisababisha kutotekelezwa kwa wakati.

“Tunasema ingewezekana, lakini kwa wakati ule taratibu na vibali vya kilojistiki viligoma. Wenzetu kule Cambodia walikosa uvumilivu wa kusubiri, wakamjengea mnara mkubwa kule,” amesema Prof. Chibunda.

Kwa hatua hiyo, Magawa aliendelea kubaki nchini Cambodia ambako alifanya kazi kubwa ya kusaidia kutambua mabomu ya ardhini na kuokoa maisha ya watu.

Historia ya Magawa inaendelea kuwa sehemu muhimu ya mafanikio ya mradi wa SUA wa kufundisha panya kwa matumizi mbalimbali, ikionyesha namna utafiti unaofanywa Tanzania unavyoweza kuzalisha matokeo yenye kutambulika kimataifa.

Mradi huo pia unaendelea kuifanya SUA kuwa miongoni mwa taasisi zinazotumia utafiti na ubunifu katika kutumia uwezo wa wanyama katika kutatua changamoto za kijamii, kiafya na kiusalama.


Na Janeth Raphael - MichuziTv - Bungeni Dodoma.


Serikali imesema imeweka mikakati mbalimbali ya kukuza vipaji na ujuzi kwa vijana wenye ulemavu, kuwawezesha kupata ajira zenye staha na kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi.

Kauli hiyo imetolewa na Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Dkt. Jafar Seif, wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Mhe. Yumna Mmanga Omar, lililohusu mkakati mahsusi wa Serikali wa kukuza vipaji na ujuzi kwa vijana wenye ulemavu ili kuongeza ajira na ushiriki wao katika uchumi.

Akijibu swali hilo, Dkt. Seif amesema Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2025–2030, hususan Kifungu cha 95, imeweka msisitizo wa kuwashirikisha na kuwawezesha watu wenye ulemavu kupata ajira zenye staha pamoja na kujenga uwezo wao ili washiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi.

Amesema Serikali pia inatekeleza Mkakati wa Kitaifa wa Kukuza na Kuendeleza Vipaji na Ujuzi kwa Vijana unaoongozwa na Sera ya Taifa ya Maendeleo ya Vijana ya mwaka 2007, Toleo la mwaka 2024.

Kwa mujibu wa Dkt. Seif, Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 nayo imeweka mkazo katika kukuza elimu jumuishi na kuhakikisha vijana wenye ulemavu wanapata fursa sawa katika elimu, mafunzo ya ufundi, ajira na shughuli mbalimbali za kiuchumi.

Amesema mikakati hiyo inalenga kuhakikisha ulemavu hauwi kikwazo kwa mtu kutumia kipaji, uwezo na ujuzi wake katika kujenga maisha yake na kuchangia maendeleo ya Taifa.

Katika utekelezaji wa mikakati hiyo, Serikali imewezesha vijana wenye ulemavu kupata mafunzo ya ufundi stadi katika maeneo mbalimbali nchini.

Dkt. Seif amesema jumla ya vijana 643 wenye ulemavu walijiunga na kuhitimu mafunzo ya ufundi stadi katika vyuo vitano, vikiwemo vya VETA, katika kipindi cha mwaka 2023 hadi 2025.

Amesema vijana hao walipata ujuzi katika fani mbalimbali zikiwemo umeme wa majumbani, useremala, uungaji vyuma, ushonaji wa nguo na viatu, kilimo na ufugaji, pamoja na ujenzi na uashi.

Mbali na mafunzo, Serikali imeendelea kuweka mazingira ya kuwawezesha vijana wenye ulemavu kutumia ujuzi walioupata katika kujiajiri na kushiriki katika uchumi.

Dkt. Seif amesema Serikali imetenga asilimia 30 ya zabuni za umma kwa ajili ya kuwawezesha makundi yanayolengwa, ambapo hadi mwaka 2024/25 jumla ya vikundi 703 vya watu wenye ulemavu vilikuwa vimesajiliwa katika mfumo wa NeST.

Hatua hiyo inalenga kuhakikisha kuwa ujuzi na vipaji vinavyopatikana kupitia mafunzo vinaweza kugeuzwa kuwa fursa za ajira, ujasiriamali na kujikwamua kiuchumi.

Aidha, Serikali imeendelea kutenga asilimia 10 ya mapato ya Halmashauri kwa ajili ya mikopo kwa makundi maalum, ambapo asilimia mbili hutengwa kwa ajili ya watu wenye ulemavu.

Katika kipindi cha mwaka 2021 hadi 2026, Serikali imesema jumla ya Shilingi bilioni 26.87 zimetolewa kwa ajili ya kuwawezesha watu wenye ulemavu kupitia mikopo hiyo.

Serikali imesisitiza kuwa hatua hizo ni sehemu ya juhudi za kuhakikisha vijana wenye ulemavu wanapata fursa sawa za kujenga vipaji, kupata ujuzi, kuajiriwa au kujiajiri na hatimaye kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya kiuchumi na kijamii ya Taifa.





Baraza la Masoko ya Mitaji linatarajia kuimarisha ushirikiano kwa kubadilishana uzoefu katika usimamizi wa kesi, utatuzi wa migogoro na matumizi ya teknolojia, huku shughuli za biashara na uwekezaji nchini zikiendelea kukua.

Ushirikiano huo utaliwezesha baraza la masoko ya mitaji ambalo ni baraza jipya, kujifunza kutokana na uzoefu wa baraza la ushindani  ambalo tangu lilipoanza kusikiliza migogoro mwaka 2007, limewahi kushughulikia zaidi ya kesi 525.

Maofisa wa taasisi hizo walijadili ushirikiano huo wakati ujumbe wa baraza la masoko ya mitaji ulipotembelea baraza la ushindani.

Akizungumza kuhusu ushirikiano huo Msajili wa baraza la ushindani Mbegu Kaskasi, alisema pia kubadilishana uzoefu kutasaidia taasisi hizo kuboresha huduma na kuhakikisha migogoro inayohusu wafanyabiashara na wawekezaji inatatuliwa ndani ya muda unaofaa.

“Tumekuwa hapa kwa karibu miaka 20. Wao wamekuja kujifunza kutokana na uzoefu wetu, lakini sisi pia tumejifunza mengi kutoka kwao licha ya kuwa wameanzishwa miaka mitatu iliyopita,” alisema.

Kaskasi alisema baraza hilo hushughulikia wastani wa kesi 45 hadi 50 kwa mwaka, zikiwamo zinazohusu bidhaa bandia na migogoro inayotokana na maamuzi ya mamlaka za udhibiti.

Alisema uzoefu huo unaweza kusaidia baraza la masoko ya mitaji kujenga mifumo bora ya usimamizi wa kesi kadri idadi ya wawekezaji na wafanyabiashara inavyoongezeka.

Kaskasi alisema utatuzi wa migogoro kwa haraka ni muhimu kwa sababu kesi zinazochukua muda mrefu zinaweza kuathiri thamani ya bidhaa na mali za kifedha.

“Ikiwa bidhaa zinashikiliwa kwa miaka miwili, zinaweza kuharibika. Kwa upande wa fedha, kama fedha zimefungwa na haziwezi kutumika kwa miaka miwili, thamani yake hupungua. Katika sekta ya fedha, muda ni kila kitu,” alisema.

Alisema lengo kuu la mabaraza hayo ni kuwezesha shughuli za biashara na kujenga mazingira bora zaidi kwa wawekezaji.

“Lengo la mabaraza haya ni kuchochea maendeleo ya nchi, kurahisisha biashara na kuvutia wawekezaji,” alisema.

Kwa upande wake, Msajili wa baraza la masoko ya mitaji Dk Martin Kolikoli, alisema taasisi hiyo ina nia ya kujifunza zaidi namna baraza la ushindani inavyopanga na kuratibu kesi ili kuhakikisha maamuzi yanatolewa kwa wakati.

baraza la masoko ya mitaji limekuwa likifanya kazi kwa takribani miaka mitatu na hadi sasa limesajili migogoro sita. Kesi mbili zilirudishwa kutokana na changamoto za kiutaratibu, tatu zimeamuliwa na moja bado inaendelea.

Dk Kolikoli alisema migogoro iliyowasilishwa hadi sasa imehusisha zaidi wawekezaji na wasuluhishi wa masoko ya mitaji, hususan madalali.

Alisema baadhi ya wawekezaji wamekuwa na malalamiko kuhusu maamuzi yaliyofanywa na madalali bila kuwashirikisha, huku wengine wakiwa na migogoro kuhusu fedha baada ya mauzo ya uwekezaji.

Alisema kujifunza kutoka kwa baraza lenye uzoefu zaidi kutaiwezesha baraza la masoko ya mitaji kujiandaa kwa ongezeko la kesi kadri ushiriki katika masoko ya mitaji unavyoendelea kukua.

Dk Kolikoli alisema baraza pia inaandaa mfumo wa usimamizi wa kesi utakaowawezesha wahusika kushiriki katika vikao kwa njia ya mtandao na kupata nakala za maamuzi bila kulazimika kufika katika baraza hilo.









Top News