Na Belinda Joseph – Dodoma

Chama cha Walimu Tanzania (CWT) kimesema kinaendelea kuimarisha huduma za utetezi kwa wanachama wake, ikiwemo kuwapatia msaada walimu wanachama wanaokabiliwa na changamoto mbalimbali za kikazi na kisheria.

Hayo yameelezwa na Kaimu Katibu Mkuu wa CWT, Protas Magesa, Septemba 2, 2026, jijini Dodoma, wakati wa kikao cha viongozi wa Chama cha Walimu Tanzania na walimu wanachama mahali pa kazi kutoka Ofisi ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, akieleza kuwa chama hicho kinatumia fedha nyingi kuhakikisha walimu wanapata huduma ya utetezi inapohitajika.

Magesa amesema CWT pia inaendelea kutekeleza miradi mbalimbali inayolenga kuwajengea uwezo walimu, ikiwemo kutoa elimu kwa walimu wenye mahitaji maalum kuhusu matumizi ya mifumo, na mwendelezo wa utekelezaji wa miradi mingine huku akisisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano kati ya chama hicho na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ili kubaini maeneo ambayo wanaweza kushirikiana katika kuwahudumia na kutatua changamoto zinazowakabili walimu.

Aidha, amesema CWT kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali imeandaa programu ya kutoa elimu kwa walimu wa sayansi ambao ni wanachama wa chama hicho kuhusu matumizi salama ya kemikali wanazotumia katika utekelezaji wa majukumu yao, amesema utoaji wa elimu hiyo unatarajiwa kuanza mwezi Oktoba mwaka huu katika Mkoa wa Mara na baadae kuendelea katika maeneo mengine nchini.

Akizungumza Afisa kutoka ofisi ya Kamishna wa Elimu Mwalimu Mbutorwe Mwakyima, amesema ushirikiano kati ya CWT na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ni muhimu katika kusikiliza na kutatua changamoto zinazowakabili walimu, amesema wanapopata haki zao na mazingira bora ya kutekeleza majukumu yao, wanaweza kufanya kazi kwa ufanisi zaidi na hivyo kuchangia katika kuboresha sekta ya elimu nchini.

Kwa upande wake, Afisa udhibiti ubora wa shule kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Bartolomeo Mwekila, amesema CWT imekuwa na mchango katika kuwasaidia walimu katika masuala mbalimbali, ikiwemo upandishaji wa madaraja, aidha ameshauri chama hicho kuendelea kuwawezesha walimu kupitia mafunzo ya mara kwa mara pamoja na kuwatafutia fursa za ajira ndani na nje ya nchi, andapo nafasi zitahitajika.







· Kiwanda Kipya cha TZS Bilioni 35 Kupunguza Uagizaji wa Bidhaa Nje

DAR ES SALAAM, Septemba 2, 2026: Serikali imezishauri kampuni zinazotoa huduma za uhandisi wa madini kubuni miradi na bidhaa zao kwa kuzingatia mahitaji ya wachimbaji wadogo na wa kati, ikisema uwekezaji wa ndani katika mnyororo wa ugavi wa sekta ya madini unapaswa kunufaisha sehemu kubwa zaidi ya wadau wa sekta hiyo.

Kamishna wa Tume ya Madini ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Ushirikishwaji wa Watanzania katika Sekta ya Madini (Local Content), Dkt. Theresia Charles Numbi, alitoa wito huo wakati wa ziara yake katika kiwanda kipya cha uzalishaji na huduma za uhandisi wa madini chenye thamani ya TZS bilioni 35 kinachojengwa na Kampuni ya Mining Engineering Services Tanzania Limited (MES), ambayo ni kampuni mwanachama wa Kundi la Makampuni la VINMART, kilichopo Kigamboni, Dar es Salaam.

Dkt. Numbi alifanya ziara katika kiwanda hicho kipya kinachojengwa kutoka hatua za awali, kwa lengo la kutathmini maendeleo ya mradi huo pamoja na mipango ya shughuli za uzalishaji. Alisema Serikali itaendelea kuunga mkono uwekezaji unaochangia ukuaji wa sekta ya madini, kuimarisha uzalishaji wa viwandani nchini na kuchochea maendeleo ya kiuchumi ya Tanzania.

Alitoa wito kwa kampuni hiyo kuhakikisha kuwa mradi huo pamoja na bidhaa zitakazozalishwa vinabuniwa kwa namna itakayowawezesha wachimbaji wadogo na wa kati katika maeneo mbalimbali nchini kunufaika na uwekezaji huo.

“Serikali itaendelea kuunga mkono uwekezaji kama huu wa MES unaolenga kuwezesha ukuaji wa sekta ya madini na kuchangia maendeleo ya kiuchumi ya nchi,” alisema Dkt. Numbi.

Kiwanda cha MES kinatarajiwa kupunguza kwa kiasi kikubwa utegemezi wa Tanzania kwa bidhaa za matumizi ya mara kwa mara katika shughuli za uchimbaji madini chini ya ardhi, ambazo kwa kiasi kikubwa zimekuwa zikiagizwa kutoka kwa wasambazaji wa nje ya nchi.

Uwekezaji huo wa TZS bilioni 35 unahusisha ujenzi wa kiwanda, mitambo pamoja na miundombinu saidizi inayohitajika kuwezesha uzalishaji wa bidhaa hizo nchini.

Kwa mujibu wa uongozi wa MES, uwekezaji huo unalenga kuchukua nafasi ya bidhaa za matumizi ya mara kwa mara katika uchimbaji wa madini chini ya ardhi, ambazo kwa sasa huagizwa kutoka nje, kwa kuzalisha bidhaa hizo hapa nchini.

Mkurugenzi Mtendaji wa MES, Bw Pulin Manek, alisema kampuni hiyo imewekeza katika uwezo mkubwa wa uzalishaji utakaokidhi mahitaji ya soko la ndani, huku ukiweka mazingira ya Tanzania kuhudumia masoko mengine ya madini katika ukanda huu.

“Sababu ya kuanzisha kiwanda hiki ni kuisaidia Tanzania kupunguza utegemezi wa bidhaa za matumizi ya mara kwa mara katika uchimbaji wa madini chini ya ardhi zinazoagizwa kutoka nje, ambazo zinaendelea kuigharimu nchi kiasi kikubwa cha fedha,” alisema Manek.

“Tumewekeza katika uwezo wa kutosha wa uzalishaji ili kukidhi mahitaji ya soko la ndani, huku tukiiweka Tanzania katika nafasi ya kuhudumia masoko mengine ya madini katika ukanda huu.” Aliongeza.

Kiwanda hicho kitakapoanza kufanya kazi kwa ukamilifu, kitakuwa na uwezo wa kuzalisha bidhaa za ‘split sets’ kwa kiwango kinachokadiriwa kuwa mara mbili na nusu ya mahitaji ya sasa ya Tanzania kwa mwezi.

“Uwezo huu unatosha kuchukua nafasi ya uagizaji wa ‘split sets’ kutoka nje, huku ukiwezesha Tanzania kuuza ziada ya bidhaa hizo katika masoko ya kikanda,” alisema Manek.

Uwezo wa kiwanda hicho wa kuzalisha ‘mine mesh’ utakuwa mkubwa zaidi, ambapo kimebuniwa kuzalisha kiasi kinachokadiriwa kuwa mara nane ya mahitaji ya sasa ya Tanzania kwa mwezi.

Manek alisema uwezo huo wa ziada umeandaliwa kwa makusudi ili kuhudumia migodi mipya ya chini ya ardhi, kusaidia migodi inayobadilisha mfumo wa uchimbaji kutoka wazi kwenda chini ya ardhi, pamoja na kukidhi mahitaji ya masoko ya nchi jirani.

“Tunazalisha zaidi ya mahitaji ya sasa ya nchi kwa sababu tunaangalia mahitaji ya baadaye ya Tanzania katika uchimbaji wa madini chini ya ardhi, pamoja na fursa zilizopo katika ukanda mpana zaidi,” alisema Manek. “Tunaamini kuwa nchi haipaswi kuendelea kuagiza bidhaa za matumizi ya mara kwa mara ambazo zinaweza kuzalishwa hapa nchini.”

Kiwanda hicho kitakuwa na njia kuu tatu za uzalishaji, ambazo ni mine mesh, friction-stabiliser split sets na dome plates. Uwekezaji wa kampuni hiyo unalenga kuhudumia sekta za nishati, usafirishaji na madini.

Kwa mujibu wa Bw Manek, MES pia ni kampuni ya kwanza nchini Tanzania kuwekeza katika mtambo wa hot-dip galvanising bath, uwekezaji unaotarajiwa kuongeza zaidi uwezo wa nchi wa kuzalisha bidhaa zinazohusiana na shughuli za madini hapa nchini.

“Mbali na kupunguza utegemezi wa bidhaa zinazoagizwa kutoka nje, mradi huu unatarajiwa kuunda fursa za ajira kwa Watanzania, hususan katika uzalishaji, uchomeleaji, galvanising na uhandisi, huku ukisaidia kuimarisha ujuzi wa kitaalamu ndani ya mnyororo wa ugavi wa sekta ya madini nchini,” aliongeza Manek.

Kampuni hiyo pia inalenga masoko ya kikanda, yakiwemo Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Zambia na Zimbabwe, ikiwa na mipango ya kutumia nafasi ya kimkakati ya Tanzania pamoja na fursa ya usafirishaji kupitia Bandari ya Dar es Salaam ili kuifanya nchi kuwa kitovu cha uzalishaji na usambazaji wa bidhaa katika ukanda huu.

Aidha, uwezo wa uzalishaji wa kiwanda hicho unatarajiwa kuiwezesha Tanzania kuhudumia soko la ndani na kuuza bidhaa zitakazozalishwa kwa ziada katika masoko ya madini ya kikanda.

Uzalishaji wa ndani unatarajiwa pia kupunguza kwa kiasi kikubwa muda wa kuwasilisha bidhaa kwa wateja. Bidhaa za matumizi ya mara kwa mara katika shughuli za uchimbaji madini zinazoagizwa kutoka nje zinaweza kuchukua kati ya wiki nane hadi 16 kufika nchini, huku MES ikitarajia bidhaa zinazozalishwa ndani ya nchi kufikishwa kwa wateja ndani ya siku chache.

Uwekezaji huo unatajwa kuendana na Sheria ya Madini ya Tanzania pamoja na Kanuni za Maudhui ya Ndani, zinazotoa kipaumbele kwa bidhaa zinazozalishwa nchini na huduma zinazotolewa na raia wa Tanzania pamoja na kampuni zilizosajiliwa nchini.

Ujenzi wa kiwanda cha MES unafanyika wakati Serikali ikiendelea na juhudi za kuongeza ushiriki wa wazawa katika mnyororo wa thamani wa madini, kuongeza uzalishaji wa viwandani nchini na kuhakikisha kuwa uwekezaji katika sekta hiyo unazalisha manufaa mapana zaidi ya kiuchumi kwa Watanzania.



Kamishna wa Tume ya Madini ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Ushirikishwaji wa Watanzania katika Sekta ya Madini (Local Content), Dkt. Theresia Charles Numbi (katikati-kushoto), akizungumza na Wakurugenzi wa Kampuni ya Mining Engineering Services Tanzania Limited (MES), kampuni mwanachama wa Kundi la Makampuni la VINMART, wakati wa ziara yake katika kiwanda cha kampuni hiyo jijini Dar es Salaam jana.
Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Mining Engineering Services Tanzania Limited (MES), Pulin Manek (katikati), akizungumza na waandishi wa habari wakati wa ziara ya Kamishna wa Tume ya Madini ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Ushirikishwaji wa Watanzania katika Sekta ya Madini (Local Content), Dkt. Theresia Charles Numbi katika kampuni hiyo jijini Dar es Salaam jana.

Na Mwandishi Wetu.

Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imekutana na kufanya mazungumzo na watangazaji na waandaaji wa kipindi cha Good Morning kinachorushwa na Wasafi FM, ambapo imewakumbusha umuhimu wa kuzingatia sheria, kanuni na maadili ya uandishi wa habari katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.

Kikao hicho kimefanyika leo, Septemba 2, 2026, katika Makao Makuu ya JAB, Mtaa wa Jamhuri, jijini Dar es Salaam, kikilenga kuimarisha uelewa wa watangazaji hao kuhusu misingi ya weledi, uwajibikaji na matumizi sahihi ya majukwaa ya habari.

Akizungumza katika kikao hicho, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa JAB, Wakili Patrick Kipangula, amefafanua matakwa ya Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229; Sheria ya Mawasiliano ya Kielektroniki na Posta, Sura ya 306; pamoja na kanuni zake zinazopaswa kuzingatiwa katika utayarishaji na utangazaji wa maudhui.

Wakili Kipangula ameeleza kuwa kuzingatia sheria na maadili ni msingi wa kulinda heshima ya taaluma, haki za watu wanaohusika katika maudhui na imani ya jamii kwa Waandishi wa Habari.

Baada ya mazungumzo hayo, watangazaji wakongwe Gelard Hando na Hilary Mtuta, maarufu kama Zembwela, walikabidhiwa vitambulisho vyao vya ithibati ya uandishi wa habari baada ya kukidhi vigezo vilivyowekwa kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari.

Makabidhiano hayo yamekamilisha hatua ya kuwatambulisha rasmi kama Waandishi wa Habari wenye ithibati, wenye wajibu wa kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa weledi, maadili na uwajibikaji. 




Waziri wa Madini, Anthony Mavunde, akizindua Programu ya Mining for a Brighter Tomorrow (MBT) katika eneo la Nyamongo, mkoani Mara, inayolenga kupanua fursa za maeneo ya uchimbaji, taarifa za kijiolojia na leseni kwa vijana, wanawake na watu wenye ulemavu.

Helikopta ikifanya utafiti wa madini kwa njia ya anga katika eneo la Nyamongo ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa Programu ya MBT, hatua itakayosaidia kupata taarifa za kijiolojia kwa ajili ya utafiti wa kina na uchorongaji katika maeneo yaliyotengwa kwa wachimbaji wadogo.



Msajili wa Hazina, Bw. Nehemiah Mchechu, amekutana na ujumbe wa kampuni ya madini ya AngloGold Ashanti kujadili maendeleo ya shughuli za kampuni hiyo na namna ya kuimarisha uhusiano wake na Tanzania.

Msajili wa Hazina, Bw. Nehemiah Mchechu, alifanya mazungumzo hayo Jumanne, Septemba 1, 2026, wakati ujumbe wa AngloGold Ashanti ulipomtembelea ofisini kwake jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kumweleza maendeleo ya shughuli za kampuni hiyo na maslahi yake ya kibiashara nchini Tanzania.

Ujumbe huo uliongozwa na Bi. Lizelle Marwick, Afisa Mkuu wa Sheria wa AngloGold Ashanti, na ulijumuisha Balozi Baso Sangqu, Makamu wa Rais Mwandamizi anayeshughulikia Uendelevu wa AngloGold Ashanti, pamoja na Bw. Simon Shayo, Makamu wa Rais anayeshughulikia Uendelevu na Ushirikishwaji wa wadau wa Geita Gold Mining Limited (GGML).

AngloGold Ashanti ni mojawapo ya kampuni kubwa duniani katika sekta ya madini na inafanya shughuli zake nchini kupitia kampuni tanzu ya GGML.

Akizungumza na ujumbe huo, Bw. Mchechu alisema OTR, kama mwakilishi wa Serikali katika umiliki wa hisa, ni mshirika mwenza wa kampuni hiyo, akisisitiza kuwa mafanikio ya biashara yana manufaa kwa pande zote mbili.

“Nyie msipopata matokeo, na sisi hatupati matokeo; na nyie mkipata matokeo, na sisi tunapata matokeo,” alisema.

Alisema OTR inafanya kazi kwa karibu na mamlaka husika, huku taasisi hizo zikiwa na mtazamo mmoja kuhusu masuala muhimu ili kutengeneza mazingira rafiki zaidi ya uwekezaji.

Bw. Mchechu alisema OTR inalenga kujenga uhusiano wa muda mrefu na AngloGold Ashanti unaozingatia uelewano, utawala bora wa kampuni na mafanikio endelevu ya biashara.

Alisisitiza pia umuhimu wa kuwa na bodi za wakurugenzi zenye watu wenye uwezo, uelewa wa biashara na mtazamo wa kimkakati, akibainisha kuwa wajumbe wa bodi wanapaswa kuwa na uwezo wa kuongeza thamani katika uendeshaji na mwelekeo wa kampuni, hususan katika taasisi zinazochangia kodi na gawio kwa Serikali.

Kwa upande wake, Bi. Marwick alisema AngloGold Ashanti inathamini uhusiano wake na Serikali za nchi ambako inafanya shughuli zake, huku akieleza kuwa kampuni hiyo inatambua umuhimu wa uhusiano wake wa muda mrefu na Serikali ya Tanzania.

Alisema kampuni hiyo inalenga kujenga ushirikiano wa kweli unaowezesha kila upande kutumia uwezo na uzoefu wake katika kutengeneza matokeo yenye manufaa kwa kampuni na nchi kwa ujumla.

Katika kuimarisha uelewa na uwezo wa wajumbe wa bodi, Bi. Marwick alisema AngloGold Ashanti iko tayari kushirikiana katika programu za mafunzo na utangulizi wa majukumu ya bodi, zitakazohusu wajibu wa wajumbe, taratibu za uendeshaji wa bodi na uelewa wa masuala ya fedha.

Pia alipendekeza wajumbe wa bodi kufanya ziara katika Mgodi wa Dhahabu wa Geita ili kupata uelewa wa moja kwa moja kuhusu shughuli za uchimbaji, pamoja na masuala ya kitaalamu yanayohusu rasilimali na akiba ya madini.

Alisema uhusiano mzuri uliopo kati ya kampuni hiyo na Serikali unaweza kuwa msingi muhimu wa kuendeleza shughuli zake katika maeneo mengine yenye leseni za utafiti nchini, kwa kuwa kampuni inaweza kupanua shughuli zake kwa urahisi zaidi katika mazingira ambayo tayari ina shughuli, miundombinu na uhusiano mzuri wa kikazi na Serikali.





Na Janeth Raphael -MichuziTv -Bungeni Dodoma 


SERIKALI imeeleza mikakati mbalimbali inayotekelezwa katika kuendeleza michezo kwa watu wenye ulemavu, ikiwemo kuandaa makocha, kuendesha mashindano na matamasha ya michezo, pamoja na kuwawezesha wanamichezo wenye ulemavu kushiriki mashindano ya kimataifa.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda, wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Nyamizi Simon Mhoja, aliyetaka kujua mkakati wa Serikali wa kuendeleza michezo kwa watu wenye ulemavu na kuzalisha wachezaji wenye ulemavu.

Waziri Makonda amesema Serikali kupitia Baraza la Michezo la Taifa (BMT) imeendelea kuchukua hatua mbalimbali kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapata fursa ya kushiriki na kuendeleza vipaji vyao katika michezo.

Amesema hatua hizo ni pamoja na kuandaa makocha wa michezo kwa watu wenye ulemavu, kuendesha matamasha yanayowashirikisha, kuandaa mashindano ya ndani ya michezo mbalimbali, pamoja na kuwezesha wanamichezo wenye ulemavu kushiriki mashindano ya kimataifa.

Aidha, Waziri Makonda amesema Serikali imeendelea kuhamasisha uanzishaji na usajili wa vyama vya michezo kwa watu wenye ulemavu, hatua inayolenga kuimarisha usimamizi na maendeleo ya michezo hiyo nchini.

Hadi Agosti 2026, jumla ya vyama tisa (9) vya michezo kwa watu wenye ulemavu vimesajiliwa, vikihusisha michezo mbalimbali ikiwemo soka, mpira wa kikapu, tenisi, riadha na kuogelea.

Hatua hizo zinaelezwa kuwa sehemu ya jitihada za Serikali za kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapata mazingira bora ya kugundua, kukuza na kutumia vipaji vyao katika michezo, ndani na nje ya Tanzania.


Na Janeth Raphael - MichuziTv- Bungeni Dodoma

SERIKALI imesema kima cha chini cha mshahara katika sekta binafsi nchini huwekwa kwa kuzingatia sekta za kiuchumi pamoja na vigezo mbalimbali vya kisheria, huku ikisisitiza kuwa utaratibu huo haujajengwa kwa lengo la kubagua wafanyakazi wa kampuni za kigeni na zile za kizawa.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano) Deus Sangu wakati akijibu swali la Mbunge wa Kuteuliwa, Mheshimiwa Abdulliah Ali Mwinyi, aliyehoji iwapo Serikali haioni kuwa utofauti wa viwango vya kima cha chini cha mshahara kati ya kampuni za kigeni na za kizawa unaweza kutengeneza tabaka katika jamii.

Katika swali lake, Mbunge huyo alitaka kujua kama Serikali haioni kuwa kanuni zinazoweka viwango tofauti vya mishahara kwa kampuni za kigeni na za kizawa zinaweza kuleta ubaguzi katika ajira na malipo ya wafanyakazi.

Akijibu, Waziri amesema kima cha chini cha mshahara kinawekwa kwa mujibu wa Sheria ya Taasisi za Kazi, Sura ya 300, ambayo imeanzisha Bodi za Kima cha Chini cha Mshahara kwa kuzingatia sekta mbalimbali za uchumi.

Waziri Sangu amesema katika Sekta Binafsi, Bodi ya Kima cha Chini cha Mshahara ina jukumu la kufanya tafiti kuhusu hali ya ajira na uchumi na kumshauri Waziri mwenye dhamana ya masuala ya kazi kuhusu kiwango kinachopaswa kuwekwa na kutangazwa kwa sekta husika.

Waziri amesema kima cha chini cha mshahara katika sekta binafsi nchini hakipangwi kwa mtazamo wa kampuni kuwa ya kigeni au ya kizawa pekee, bali huzingatia sekta za kiuchumi ambazo waajiri na wafanyakazi wanafanyia kazi.

Aidha, amesema katika kupanga viwango hivyo, Serikali huzingatia vigezo mbalimbali vilivyowekwa na mikataba ya kimataifa pamoja na sheria za nchi, ikiwemo uwezo wa waajiri kufanya biashara na kulipa ujira unaostahili.

Kigezo kingine kinachozingatiwa, kwa mujibu wa Serikali, ni gharama za maisha, jambo linalolenga kuhakikisha viwango vya mishahara vinazingatia mazingira halisi ya kiuchumi yanayowakabili wafanyakazi na waajiri.

Kauli hiyo ya Serikali imekuja wakati ambapo suala la tofauti za mishahara katika sekta binafsi likiwa miongoni mwa hoja zinazogusa usawa katika ajira, uwezo wa waajiri na ustawi wa wafanyakazi.

Serikali imeendelea kusisitiza kuwa upangaji wa kima cha chini cha mshahara unapaswa kuzingatia hali ya uchumi, gharama za maisha na uwezo wa waajiri, huku ukiendana na matakwa ya sheria za nchi na mikataba ya kimataifa ya kazi.



-Ni katika Wiki ya Ubunifu Tanzania (IWTz) 2026

Katika Wiki ya Ubunifu Tanzania (IWTz) 2026, Vodacom Tanzania imeonyesha mchango wa mtandao, ubunifu na ujasiriamali katika kufanikisha Dira ya Maendeleo Tanzania 2050. Tukio hilo limewakutanisha wabunifu, wajasiriamali, watunga sera, wawekezaji, vijana na wadau mbalimbali chini ya kauli mbiu: “Kutoka Matarajio hadi Mageuzi: Kuibua Njia ya Tanzania Kuelekea Ustawi Jumuishi.”

Vodacom imeshiriki katika mjadala kuhusu uchumi wa watengeneza maudhui, maonesho, mikutano na wadau na shughuli za kuelimisha kuhusu usalama wa mtandao.

Akizungumza katika mjadala wa watengeneza maudhui na majukwaa mtandaoni, Mkuu wa Idara ya Chapa na Mawasiliano wa Vodacom Tanzania, Yvonne Maruma, alisema mtandao una thamani zaidi kupitia fursa unazowawezesha Watanzania kuzipata katika elimu, biashara na ubunifu.

Kupitia Vodacom Youth Base (VYB), kampuni inaendelea kuwawezesha watengeneza maudhui kubaki mtandaoni na kukuza shughuli zao za kidijitali. Ushiriki wa Vodacom katika IWTz 2026 unaunga mkono malengo ya Dira ya Maendeleo 2050 kupitia mageuzi ya kidijitali, uvumbuzi na ukuaji wa uchumi jumuishi.
Mkuu wa Idara ya Chapa na Mawasiliano wa Vodacom Tanzania Yvonne Maruma akizungumza katika Wiki ya Ubunifu Tanzania 2026 ambapo alizungumzia namna ya Vodacom inavyounganisha Watanzania na kuleta tija kupitia Zaidi ya Mtandao: Hususani Watengeneza maudhui na Majukwaa Mtandaoni kwa kuwapa mtandao bora na simu janja zinazo unga mkono ubunifu wao.

Mkuu wa Idara ya Chapa na Mawasiliano wa Vodacom Tanzania Yvonn Maruma (kulia) akisalimiana na Naibu Katibu Mkuu wa Tume ya Taifa ya Mipango Dr. Blandina Kilama baada ya kumaliza majadiliano ya namna ya kuziunganisha sauti za Watanzania: Watengeneza maudhui na Majukwaa Mtandaoni. Tukio hilo limefanyika katika Wiki ya Ubunifu Tanzania leo hii.

Mkuu wa Idara ya Chapa na Mawasiliano wa Vodacom Tanzania Yvonne Maruma (kulia) akisalimiana na Mhariri Mtendaji mkuu wa kampuni ya Mwananchi Communications Limited baada ya kumaliza majadiliano ya namna ya kuziunganisha sauti za Watanzania: Watengeneza maudhui na Majukwaa Mtandaoni. Tukio hilo lilifanyika katika Wiki ya Ubunifu Tanzania leo hii.

Mkuu wa Idara ya Chapa na Mawasiliano wa Vodacom Tanzania Yvonne Maruma (wa pili kushoto), akisikiliza majadiliano yaliyohusu namna ya kuziunganisha sauti za Watanzania: Watengeneza maudhui na Majukwaa Mtandaoni. Tukio hilo lilifanyika wakatib wa Wiki ya Ubunifu Tanzania.

Mkuu wa Idara ya Chapa na Mawasiliano wa Vodacom Tanzania Yvonne Maruma (kulia), Mkurugenzi Mtendaji wa Mwananchi Communications Limited Rosalynn Mndolwa-Mworia (wa pili wa kushoto), Meneja wa Uchunguzi wa Vodacom Tanzania Joseph Mnyune (kushoto) na Meneja Biashara Ofisi ya Mkurugenzi Mtendaji wa Mwananchi Communication Limited Tess Aloyce (wa pili kulia) wakizungumza wakati wa Wiki ya Ubunifu Tanzania ambapo Vodacom Tanzania walishiriki katika majadiliano ya namna ya kuziunganisha sauti za Watanzania: Watengeneza maudhui na Majukwaa Mtandaoni. Tukio hilo lilifanyika katika Wiki ya Ubunifu Tanzania leo hii.


 

 

Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) imetangaza kushuka kwa bei za bidhaa za mafuta kwa mwezi Septemba 2026. Bei ya petroli imeshuka kwa Shilingi 102 kwa lita, huku bei ya dizeli ikishuka kwa Shilingi 101 kwa lita. Bei hizo zitaanza kutumika kuanzia tarehe 2 Septemba 2026, saa 6:01 usiku.

EWURA inaendelea kufuatilia kwa karibu mwenendo wa bei za mafuta katika soko la dunia, ambapo mabadiliko ya bei yanaendelea kuathiriwa pamoja na mambo mengine na hali ya kiusalama katika eneo la Mashariki ya Kati.

Kwa mujibu wa Sheria ya Mafuta ya Mwaka 2015, bei za mafuta zinaendelea kupangwa kwa kuzingatia mfumo wa soko. Wafanyabiashara wote wa rejareja wanatakiwa kuuza mafuta kwa bei zisizozidi bei elekezi, na wananchi wanashauriwa kutoa taarifa EWURA kwa kituo chochote cha mafuta kitakachouza zaidi ya bei elekezi.


‎JUKWAA Huru la Wahariri Tanzania (JUWATA) na Umoja wa Klabu za Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC) wamekubaliana kuimarisha ushirikiano katika kulinda uhuru wa vyombo vya habari, kutetea haki na maslahi ya waandishi wa habari pamoja na kuhakikisha jamii inapata habari sahihi na kwa wakati.

‎‎Makubaliano hayo yamefikiwa katika kikao cha pamoja cha viongozi wa JUWATA na UTPC kilichofanyika katika ofisi za UTPC zilizopo Barabara ya Aboud Jumbe, Mtaa wa Kazembo, eneo la Uzunguni jijini Dodoma.

‎Katika kikao hicho, viongozi hao walijadili masuala mbalimbali yanayohusu sekta ya habari, ikiwemo umuhimu wa kuwa na mshikamano miongoni mwa wadau wa habari katika kukabiliana na changamoto zinazowakabili waandishi wa habari na vyombo vya habari nchini.

‎Aidha, walisisitiza umuhimu wa taasisi hizo kushirikiana katika kutetea uhuru wa vyombo vya habari, haki za waandishi wa habari na maslahi yao, huku wakitambua nafasi muhimu ya wanahabari katika kuhabarisha, kuelimisha na kuwajibika katika jamii.

‎Ushirikiano huo pia unalenga kuongeza nguvu katika kushughulikia changamoto zinazohusu mazingira ya kazi ya waandishi wa habari, pamoja na kujenga mahusiano mazuri kati ya wadau wa habari na taasisi mbalimbali zinazohusika na maendeleo ya sekta hiyo.

‎UTPC ina jumla ya Klabu 28 za Waandishi wa Habari zinazowakilisha waandishi wa habari kutoka Tanzania Bara na Zanzibar, hivyo kuwa na mtandao mpana wa kuwafikia wanahabari katika maeneo mbalimbali nchini.

‎Kwa upande wa JUWATA, ujumbe uliongozwa na Mwenyekiti wake, Richard Mwaikenda, akifuatana na Makamu Mwenyekiti, Sylivester Ngombaniza, pamoja.

‎UTPC iliwakilishwa na Mkurugenzi Mtendaji, Kenneth Simbaya, pamoja na Afisa wa Programu wa Ufuatiliaji Rasilimali, Andrew Malawiti, Kaimu Afisa wa Fedha Winfrida Madeni na Afisa Msaidizi wa Programu, Edmund Kapungu.

‎Viongozi hao wameeleza umuhimu wa kuendeleza mawasiliano na ushirikiano wa karibu baina ya taasisi hizo kwa manufaa ya waandishi wa habari, vyombo vya habari na jamii kwa ujumla.

‎Wamesisitiza kuwa mshikamano wa wadau wa habari ni muhimu katika kujenga sekta imara, yenye weledi na inayoweza kutekeleza kwa ufanisi wajibu wake wa kuhabarisha umma na kulinda maslahi mapana ya jamii.


‎ ...........,...............


‎Jukwaa Huru la Wahariri Tanzania (JUWATA) limeanzishwa kihalali kwa kuzingatia Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, likiwa na lengo la kupanua wigo kwa Wahariri wanaotimiza vigezo kuwa huru kujiunga na jukwaa hilo, ili kuongeza nguvu, umoja na ushirikiano katika kutetea na kulinda haki na maslahi ya Waandishi wa Habari pamoja na jamii kwa ujumla.

‎Katika kutekeleza majukumu yake ya kila siku, JUWATA itazingatia Katiba na kanuni zake, sambamba na kufuata na kuheshimu Sheria za Nchi pamoja na taratibu zinazotawala tasnia ya Habari.

‎Kwa ufupi, JUWATA haijaasisiwa kwa lengo la kupambana, kushindana au kusigana na taasisi nyingine za Habari.

‎Badala yake, inalenga kujenga ushirikiano, mshikamano na mahusiano mema na taasisi za Habari za ndani na nje ya nchi, kwa manufaa ya Wahariri, Waandishi wa Habari na jamii kwa ujumla.

‎JUWATA inaamini kuwa umoja, ushirikiano na kuheshimiana ndiyo msingi wa kujenga tasnia imara, huru, yenye uwajibikaji na inayoweza kusimamia kwa ufanisi haki na maslahi ya Wadau wa Habari.
Mkurugenzi Mtendaji wa Umoja wa Klabu za Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC, Kenneth Simbaya (katikati) akiwa na Mwenyekiti wa Jukwaa Huru la Wahariri Tanzania (JUWATA. Richard Mwaikenda pamoja na Makamu Mwenyekiti wa jukwa hilo, Sylivester Ngombaniza baada ya kufanya kikao hicho.
Kutoka kushoto ni Makamu Mwenyekiti wa JUWATA,Ngombaniza,Kaimu Afisa wa Fedha, Winfrida Madeni, Mwenyekiti wa JUWATA, Mwaikenda, Mkurugenzi Mtendaji wa UTPC, Simbaya na Afisa wa Programu UfuatiliajiRasilimali, Andrew Malawiti.
Viongozi wa JUWATA na UTPC wakiwa katika kikao hicho.

Mwaikenda akimsikiliza kwa makini Simbaya wakati wa kikao hicho.

Mwaikenda akizungumza wakati wa kikao hicho.
Simbaya akiagana na viongozi wa JUWATA.


Top News