NA: MWANDISHI WETU


Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake wa Chama Cha Mapinduzi (UWT) Taifa, na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu (MCC), Mary Chatanda, amebadilishwa mkoa wa ulezi wa kichama na sasa ni mlezi wa CCM mkoa wa Mara.

Mabadiliko hayo yamefanyika Julai 29, 2026, Zanzibar, kufuatia vikao vya Chama vinavyoendelea. Kabla ya mabadiliko hayo, Chatanda alikuwa mlezi wa mikoa ya Mjini na Magharibi, Zanzibar.

Akizungumzia mabadiliko hayo, Chatanda amekishukuru Chama chake kwa kuendelea kumuamini kutekeleza majukumu mbalimbali ya kichama.

"Nimepokea taarifa hii ya mabadiliko ya ulezi wa Chama mkoa kwa moyo wa unyeyekevu. Nakishukuru Chama changu kwa kuniamini. Niwaombe wanachama wenzangu na wananchi kwa ujumla tushirikiane kuhakikisha tunasukuma mbele gurudumu la maendeleo na Chama chetu".

Ameongeza kuwa "Serikali ya CCM chini ya uongozi wa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan imepeleka fedha nyingi za miradi ya maendeleo mkoani Mara, ni wajibu wetu kuhakikisha fedha hizo zinatumika kama ilivyokusudiwa katika kuboresha maisha ya wananchi". 

Akiwa mlezi mkoani humo, pamoja na mambo mengine, Chatanda anawajibika kuwaunganisha wanachama wa CCM na wananchi kwa ujumla.

Aidha, kuimarisha uhai wa Chama, kuongeza idadi ya wanachama na kuhimiza utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ili kuongeza kasi ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Vilevile, anawajibika kujenga uhusiano mzuri baina ya Chama na serikali.

Mkoa wa Mara unaundwa na wilaya za Bunda, Butiama, Musoma, Rorya, Serengeti na Tarime.



Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Mjumbe wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) na Kaimu Meneja wa Huduma za Kiswahili wa Shirika la Magazeti ya Serikali (TSN), Mgaya Kingoba, amesema uhuru wa kutoa maoni una mipaka ya kisheria na kimaadili, hivyo haupaswi kutumiwa kutoa matusi, kudhalilisha wengine, kuchochea chuki au kusambaza taarifa zisizo sahihi.

Kingoba amesema hayo leo, Julai 30, 2026, alipowasilisha mada kuhusu “Kuimarisha Uzalendo katika Uandishi wa Habari ili Kulinda Amani, Umoja na Mshikamano” katika siku ya pili ya mafunzo kwa watumishi wa Bongo FM, redio dada ya TBC (Shirika la Utangazaji Tanzania), yaliyofanyika katika Ofisi za JAB jijini Dar es Salaam kuanzia Julai 29, 2026.

Amesema ukosoaji ni sehemu muhimu ya uhuru wa kujieleza, lakini unapaswa kulenga kuonesha kasoro na kuchochea maboresho badala ya kushambulia watu, kutumia lugha ya kejeli au kubomoa imani ya jamii kwa taasisi.

“Mkosoaji mzalendo hafichi makosa, lakini pia hatumii matusi, kejeli au upotoshaji. Anakosoa kwa ukweli, ushahidi na lugha ya staha, akiwa na lengo la kujenga na kuboresha,” amesema Kingoba.

Ameeleza kuwa mkosoaji mzalendo hujenga ukosoaji wake katika misingi ya ukweli, ushahidi, muktadha, lugha ya staha, maslahi ya umma na mapendekezo ya suluhisho.

Aidha, amewataka watangazaji kutambua kuwa uhuru wa kujieleza hauondoi wajibu wao wa kulinda utu wa watu, amani na mshikamano wa kitaifa.

Kingoba amesema uzalendo katika utangazaji hauishii katika kuipenda nchi kwa maneno, bali unapaswa kuonekana katika maamuzi ya kitaaluma yanayolinda ukweli, umoja, amani na maslahi ya Taifa na kwamba uchaguzi wa maneno na namna ya kuendesha mijadala ya moja kwa moja unaweza kujenga jamii au kusababisha migawanyiko.

Akiwasilisha mada kuhusu Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa JAB, Wakili Patrick Kipangula, amesema Sheria hiyo inatambua uhuru wa Waandishi wa Habari na vyombo vya habari katika kutafuta, kuhariri, kuchapisha na kutangaza habari, lakini inaweka pia wajibu wa kuzingatia sheria, maadili, weledi na haki za wengine.

Amesema uhuru wa habari na uwajibikaji vinapaswa kwenda pamoja ili kulinda taaluma, maslahi ya jamii na Taifa.

Mafunzo hayo yanalenga kuwaongezea washiriki uelewa kuhusu Sheria ya Huduma za Habari, maadili ya uandishi wa habari, uzalendo na wajibu wa watangazaji katika kutumia uhuru wa kujieleza kwa weledi na uwajibikaji.













Na George Maziku, Nyang'hwale


MGODI wa wachimbaji wadogo wa dhahabu wa Mwamakiliga, unaopatikana Kijiji cha Mwamakiliga, kata ya Izunya, wilaya ya Nyang'hwale, Mkoani Geita umewawezesha zaidi ya watanzania 6000 kujiajiri kwenye kazi mbalimbali mgodini hapo na kujipatia kipato.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake mgodini hapo, Meneja msaidizi wa mgodi huo Mashaka Kulwa Chitela amesema wananchi kutoka ndani na nje ya wilaya ya Nyang'hwale na mkoa wa Geita wamenufaika kwa kujipatia kazi mbalimbali.

Amesema kuwa wananchi hao wanajishughulisha na kazi za uchimbaji, uokotaji wa mawe ya dhahabu(maarufu ukwale), biashara ya mitambo ya kusaga mawe (crushers), ubebaji wa mifuko ya mawe, boda boda, mama lishe, biashara ya nyumba za kupangisha, maduka, na nyingine nyingi.

"Mgodi wetu umeisaidia sana serikali katika kupunguza idadi ya watanzania wasio na ajira, hapa kuna umati wa zaidi ya watu 6000 wanaojipatia riziki zao za Kila siku. Wapo wachimbaji, kina mama wa ukwale, makago wanaobeba na kupakia mifuko ya mawe, boda boda, mama lishe, wenye gesti, maduka na wafanyabiashara wengine wengi", amesema Chitela.

Ameongeza kuwa, "Tumetengeneza ajira za uhakika zaidi ya 100 katika kada za ukaguzi, ulinzi, ulipuaji na uhudumu wa ofisi. Tuna imani kubwa kwamba tukipata leseni ya uchimbaji tutazalisha ajira Nyingi zaidi."

Amebainisha miongoni mwa watu walionufaika na mgodi huo ni wakazi wa kijiji cha Mwamakiliga na kata ya Izunya ambao wamekuwa wakipewa kipaumbele katikà nafasi mbalimbali za kazi zinazojitokeza mgodini hapo.

" Tumekuwa na upendeleo maalum kwa wananchi wa kijiji hiki ambao ni wenyeji wetu, walinzi wengi wa mgodi wetu wanatoka hapa Mwamakiliga. Pia tumechukua vijana 25 wa hapa kijijini na Kisha kuwafundisha kazi ya ukaguzi wa migodi", amesitiza Chitela.

Amefafanua mbali na kuzalisha ajira hizo, mgodi wake umekuwa chanzo cha uhakika cha mapato ya halmashauri ya wilaya ya Nyang'hwale kupitia ushuru mbalimbali ikiwemo ushuru wa huduma.

Amesema hata Serikali kuu imekuwa ikinufaika na uwepo wa mgodi huo kupitia malipo ya mrabaha, ambayo ni asilimia 3 kwa kila mifuko 100 ya mawe yenye dhahabu.

"Serikali imetuamini na kutukabidhi jukumu la kusimamia na kukusanya mapato yake katika mgodi huu, kazi hiyo tumekuwa tukiifanya kwa uaminifu mkubwa. Halmashauri yetu ya Nyang'hwale na serikali kuu wote wanapata mapato yao bila ubabaishaji", amebainisha Chitela.

Kuhusu usalama wa mgodi wake kwa wachimbaji na watu wengine wanaofanya kazi mgodini hapo, Chitela amesema suala la usalama kwao ni kipaumbele namba moja, na kwamba mgodi huo haujawahi kupata ajali yoyote kubwa kutokana na umakini wao mkubwa katika usalama.

"Mgodi wetu ni salama kabisa, kwetu suala la usalama ni kipaumbele cha kwanza na idara yetu ya ukaguzi ina watu wa kutosha na makini. Ukaguzi wa duara unafanyika wakati wote mchana na usiku, masaa 24 na mara ikibainila kama duara fulani ni hatarishi, tunasimamisha moja uchimbaji mpaka marekebisho yafanyike",amesema.






Victor Masangu,Bagamoyo


Mwenyekiti wa Jumuiya ya ya Wazazi Taifa Ndg. Fadhili Maganya amewasa viongozi wa CCM kuhakikisha kwamba wanavalia njuga na kusimamia ipasavyo suala la mikopo ya asilimia kumi ambayo inatolewa na Halmashauri.

Kauli hiyo ameitoa wakati wa ziara yake ya kikazi Wilaya ya Bagamoyo yenye lengo la kuona uhai wa chama pamoja na kuimarisha jumuiya zake zote sambamba na tenbelea miradi ya maendeleo.

Mwenyekiti huyo amebainisha kwamba kumekuwepo na baadhi changamoto ya utoaji wa fedha ambazo zinatolewa na mfuko wa Tasaf aziwafikii walengwa na zinakwenda kwa watu wengine ambao hawastahili

"Kuna malalamiko mengi ambayo yamekuwa yakitolewa na wananchi kuhusiana na suala la utoaji wa fedha ambazo zinatolewa na mfuko wa Tasaf zinakwenda kwa watu wengine ambao hawahusiki kabisa,"amebainisha Mwenyekiti huyo.

Kadhalika amesema kwamba fedha za asilimia kumi ambazo zinatolewa kwa ajili ya makundi ya vijana,walemavu na wanawake zinatakiwa kutolewa kwa walengwa na sio kupewa watu wengine.

Akiwa katika chuo cha uuguzi na ukunga Mwenyekiti huyo amewahimiza wanafunzi hao kuzingatia maadili pamoja na kuwa wazalendo na nchi yao.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo Shaibu Ndemanga amempongeza Mwenyekiti huyo wa Taifa kwa kufanya ziara hiyo ambayo itaweza kuleta matokeo chanya ya kimaendeleo.

Pia Mkuu huyo wa Wiaya amebainisha kuwa serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 27 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbali mbali ya maendeleo ikiwemo ujenzi wa bandari.

Naye Mwenyekiti wa chama cha mapinduzi (CCM) Wilaya ya Bagamoyo Abubakari Mlawa amebainisha kwamba bado kuna changamoto ya migogoro ya ardhi katika baadhi ya maeneo na kwamba wameshaanza kuifanyia kazi.

Mbunge wa Jimbo la Bagamoyo Subira Mgalu ameamua kutoa kiasi cha shilingi milioni 5 kupitia mfuko wa Jimbo kwa ajili ya kuweza kukarabati miundombinu ya majengo pamoja na uzio katika chuo cha uuguzi na ukunga Bagamoyo.

Mwenyekiti wa wazazi Mkoa wa Pwani Jackson KItuka amesema wataendelea kushirikiana na viongozi mbali mbali wa chama na serikali kwa ajili ya kuleta maendeleo.

Ziara ya Mwenyekiti wa Jumuiya ya wazazi ya CCM Taifa imeendelea katika Wilaya ya Bagamoyo ambapo imetembelea miradi mbali mbali ya maendelo ikiwemo chuo cha uuguzi na ukunga,chuo cha kilimo kaole,kiwanda cha kuchakata taka hatarishi pamoja na miradi mbali ikiwemo Hospitali ya Chalinze na sekta ya elimu.



Na Said Mwishehe, Michuzi TV

SERIKALI kwa kushirikiana na Shirika la Umoja wa Mataifa la Maendeleo (UNDP), Umoja wa Ulaya (EU) na Ubalozi wa Ireland imezindua awamu ya nne ya ufadhili wa masomo ya nishati endelevu kwa wanawake 15 nchini.

Hatua hiyo itafanya idadi ya wanufaika wa mpango wa Women in Sustainable Energy (WISE) kufikia 60 tangu ulipoanzishwa mwaka 2023 kwa ushirikiano kati ya Wizara ya Nishati na Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT), ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuongeza ushiriki wa wanawake katika sekta ya nishati.

Akizungumza katika uzinduzi wa dirisha la maombi jijini Dar es Salaam, mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Emilian Nyanda, amesema Serikali inawekeza katika maendeleo ya rasilimali watu ili kuhakikisha nchi inakuwa na wataalamu wa kutosha wa kusimamia mabadiliko ya sekta ya nishati.

Amesema Tanzania inaendelea kutekeleza mikakati ya kuongeza uzalishaji wa umeme, kuimarisha matumizi ya nishati jadidifu, matumizi bora ya nishati na ajenda ya nishati safi ya kupikia, lakini mafanikio ya mipango hiyo yanategemea pia upatikanaji wa wataalamu wenye ujuzi.

"Haya si masomo pekee; ni uwekezaji wa moja kwa moja katika wataalamu watakaosimamia sera, teknolojia na ubunifu utakaoiwezesha Tanzania kufikia malengo yake ya maendeleo ya sekta ya nishati," amesema.

Nyanda amesema wahitimu wengi wa awamu tatu zilizopita tayari wamepata ajira katika Wizara ya Nishati, TANESCO, taasisi za utafiti na kampuni binafsi, huku wengine wakianzisha biashara zinazotoa huduma za kitaalamu katika sekta hiyo.

Amefafanua programu hiyo pia inaunga mkono utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Mkakati wa Nishati Safi ya Kupikia na mpango wa Mission 300 unaolenga kuongeza upatikanaji wa umeme kwa Waafrika milioni 300 ifikapo mwaka 2030.

Kwa upande wake, Meneja wa Maendeleo ya Vipaji wa UNDP Tanzania, Veronica Sigala, amesema mpango wa WISE unalenga kuwawezesha wanawake vijana kupata elimu ya juu na ujuzi wa kitaalamu utakaowawezesha kushiriki kikamilifu katika mabadiliko ya sekta ya nishati.

Amesisitiza mpango huo unachangia utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs), ikiwemo elimu bora, usawa wa kijinsia, nishati safi na nafuu, ajira zenye staha na hatua dhidi ya mabadiliko ya tabianchi.

"Tanzania haiwezi kufanikisha mabadiliko ya sekta ya nishati kupitia miundombinu, sera na fedha pekee. Tunahitaji watu wenye ujuzi, na wanawake lazima wawe miongoni mwa wahandisi, watafiti, wabunifu na viongozi wa mabadiliko hayo," amesema.

Kwa upande wake Mkuu wa Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam(DIT), Profesa Preksedis Ndomba, amesema programu hiyo inaendana na maono ya taasisi ya kutumia elimu, utafiti na ubunifu kutatua changamoto za maendeleo ya taifa.

Amesema DIT imeongeza idadi ya wanafunzi wanawake katika taaluma za uhandisi kutoka asilimia 14 mwaka 2016 hadi asilimia 25 kwa sasa, huku ikilenga kufikia asilimia 35 mwaka 2031 na uwiano wa asilimia 50 kwa 50 ifikapo mwaka 2050.

Prof.Ndomba amesema zaidi ya asilimia 60 ya mafunzo yanayotolewa chuoni hapo ni ya vitendo kupitia mfumo wa Teaching Factory, hatua iliyowezesha zaidi ya asilimia 70 ya wahitimu kupata ajira au kujiajiri ndani ya miezi sita baada ya kuhitimu.

Amewahimiza wanawake wenye sifa kutumia fursa hiyo ya ufadhili, akisema kuongeza ushiriki wao katika sekta ya nishati kutasaidia kuimarisha ubunifu, kuongeza nguvu kazi yenye ujuzi na kuharakisha maendeleo ya uchumi wa Tanzania.






Na. Ramadhani Kissimba, Durban

Nchi wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) zimeshauriwa kuimarisha ushirikiano na kuweka mikakati ya pamoja itakayochochea maendeleo ya viwanda pamoja na kuongeza mnyororo wa thamani wa bidhaa zinazozalishwa katika ukanda huo.

Ushauri huo umetolewa na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Maendeleo TIB, Bw. Deogratius Kwiyukwa, kando ya Mkutano wa 9 wa Wiki ya Viwanda wa SADC (SADC Industrialisation Week) unaoendelea jijini Durban, Afrika Kusini.

Akizungumza kuhusu mijadala ya mkutano huo, Bw. Kwiyukwa alisema moja ya ajenda kuu ni namna nchi wanachama zitakavyowekeza katika viwanda vya kuongeza thamani ya bidhaa zinazozalishwa ndani ya ukanda wa SADC, hususan madini ya kimkakati (critical minerals), badala ya kuendelea kuuza nje ya nchi madini hayo yakiwa katika hali ghafi.

“Jambo kubwa lililojadiliwa ni namna ya kuyaongezea thamani madini ya kimkakati katika nchi yanakopatikana madini hayo ndani ya ukanda huu kabla ya kuuzwa katika masoko ya nje,” alisema Bw. Kwiyukwa.

Alibainisha kuwa mkutano huo umefungua fursa mpya za ushirikiano miongoni mwa nchi wanachama, zikiwemo fursa za kuandaa mikakati ya pamoja itakayosaidia kufanikisha malengo ya maendeleo ya viwanda na uchumi yaliyowekwa na SADC.

Aidha, Bw. Kwiyukwa alizishauri nchi wanachama kuhakikisha sera na mipango yao ya maendeleo inaendana na dira na mikakati ya SADC ili kuharakisha utekelezaji wa miradi ya maendeleo yenye manufaa ya pamoja kwa ukanda huo.

Kwa upande wa Benki ya Maendeleo (TIB), Bw. Kwiyukwa alisema taasisi hiyo imeshiriki katika mkutano huo kwa lengo la kutafuta fursa za kushirikiana na taasisi nyingine za kifedha ndani ya ukanda wa SADC ili kuunganisha mitaji kwa ajili ya kufadhili miradi mikubwa ya maendeleo.

“Kama TIB, tumeshiriki katika mkutano huu kwa lengo la kujenga ushirikiano na taasisi nyingine za kifedha ili kuunganisha mitaji itakayowezesha kufadhili miradi mikubwa ya maendeleo inayotekelezwa na nchi wanachama wa SADC,” aliongeza Bw. Kwiyukwa.

Vilevile, Bw. Kwiyukwa alisisitiza umuhimu wa nchi wanachama kutafsiri kwa vitendo maazimio ya mkutano huo kwa kuwekeza katika sekta zinazozalisha ajira, hususan kwa vijana, ili waweze kutumia kikamilifu fursa za kiuchumi zinazopatikana ndani ya ukanda wa SADC.

Mkutano wa 9 wa Wiki ya Viwanda wa SADC umewakutanisha viongozi wa serikali, sekta binafsi, wawekezaji, taasisi za kifedha, wataalamu na wadau wa maendeleo kutoka nchi wanachama wa SADC. Mkutano huo unafanyika chini ya kaulimbiu isemayo: “Kukuza Viwanda Imara, Endelevu na Jumuishi kupitia Maendeleo ya Miundombinu, Mageuzi ya Kilimo na Madini kwa Ajili ya Dunia Yenye Haki.”

Kwa ujumla, mijadala ya Mkutano wa Wiki ya Viwanda wa SADC jijini Durban imeweka msisitizo mkubwa katika kuimarisha ushirikiano wa kikanda, kuongeza thamani ya rasilimali za madini na bidhaa nyingine kabla ya kuuzwa nje, pamoja na kuhamasisha uwekezaji katika viwanda, miundombinu na miradi ya maendeleo. Hatua hizi zinatarajiwa kuongeza ushindani wa uchumi wa ukanda wa SADC, kuvutia uwekezaji, kuimarisha biashara ya ndani ya ukanda na kuzalisha ajira zaidi, hususan kwa vijana.




Mchumi kutoka Wizara ya Fedha, Bi. Jesca Mboho, akifuatilia kwa makini mijadala inayoendelea katika Mkutano wa 9 wa Wiki ya Viwanda wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC Industrialisation Week), unaofanyika jijini Durban, Afrika Kusini.






Meneja wa Utafiti na Biashara kutoka Benki ya Maendeleo (TIB), Dkt.Hilderbrand Shayo (kushoto), akiwa katika mazungumzo na Afisa Usimamizi Mkuu wa Fedha kutoka Wizara ya Fedha, Bi. Emerensiana Nyanda (katikati), pamoja na Mchumi kutoka Wizara ya Fedha, Bi. Jesca Mboho, mara baada ya kumalizika kwa vikao vya Mkutano wa 9 wa Wiki ya Viwanda wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), unaoendelea jijini Durban, Afrika Kusini.






Meneja wa Utafiti na Biashara wa Benki ya Maendeleo Tanzania (TIB), Dkt. Hilderbrand Shayo, akitoa mchango wake wakati wa mijadala katika Mkutano wa 9 wa Wiki ya Viwanda wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC Industrialisation Week), unaoendelea jijini Durban, Afrika Kusini.






Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Maendeleo (TIB), Bw. Deogratius Kwiyukwa (katikati), akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya washiriki wa Mkutano wa 9 wa Wiki ya Viwanda wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC Industrialisation Week), unaofanyika jijini Durban, Afrika Kusini.







Afisa Sheria kutoka Tume ya Ushindani (FCC), Bw. Goerge Chananga akielezea ubora, matumizi na fursa za kiuchumi za mkonge unaozalishwa nchini Tanzania kwa mmoja wa wadau waliotembelea Banda la Tanzania, pembezoni mwa Mkutano wa Wiki ya Viwanda wa SADC (SADC Industrialisation Week 2026), unaofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano (ICC), jijini Durban, Afrika Kusini.



(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini Wizara ya Fedha-Durban)






Na Janeth Raphael - MichuziTv

Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) imetangaza mkakati mpya wa kuongeza kasi ya uwekezaji katika sekta za kilimo, mifugo na uvuvi kupitia upanuzi wa huduma za kifedha, matumizi ya teknolojia za kisasa na ushirikiano na wadau mbalimba li, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha uchumi wa Taifa na kuunga mkono utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma leo Julai 30, 2026, Mkurugenzi Mwendeshaji wa TADB, Frank Nyabundege, amesema benki hiyo imejipanga kuongeza mchango wake katika kukuza uzalishaji wa kibiashara kwa kuhakikisha wakulima, wafugaji na wavuvi wanapata mitaji inayowawezesha kuongeza tija, kutumia teknolojia za kisasa na kuwekeza katika shughuli zenye thamani kubwa zaidi.

Amesema mafanikio yaliyofikiwa na TADB katika miaka ya hivi karibuni yamechangiwa kwa kiasi kikubwa na kuimarishwa kwa mtaji wa benki kupitia Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, hatua ambayo imeongeza uwezo wa taasisi hiyo kuwafikia wanufaika wengi zaidi nchini.

Kwa mujibu wa Nyabundege, ongezeko hilo la mtaji limeiwezesha TADB kuongeza kiwango cha utoaji wa mikopo, ambapo zaidi ya asilimia 73 ya mikopo yote iliyotolewa katika kipindi cha miaka mitano ilitolewa kati ya mwaka 2022 na 2025, jambo linaloonyesha kasi ya ukuaji wa huduma za benki hiyo.

Mbali na mtaji unaotolewa na Serikali, amesema TADB imefanikiwa kuvutia fedha kutoka kwa taasisi mbalimbali za maendeleo duniani, hatua iliyoongeza uwezo wa kufadhili miradi mikubwa ya uzalishaji, uchakataji na uongezaji thamani wa mazao ya kilimo, mifugo na uvuvi.

Akizungumzia mwaka wa fedha 2026/2027, Nyabundege amesema benki hiyo itaelekeza nguvu zaidi katika kuongeza upatikanaji wa mitaji kwa sekta za uzalishaji, kuimarisha minyororo ya thamani ya mazao ya kimkakati, kuongeza ushindani wa bidhaa za kilimo katika masoko ya ndani na nje ya nchi pamoja na kupunguza utegemezi wa bidhaa zinazoagizwa kutoka mataifa mengine.

Pia amesema TADB itaendelea kuwekeza katika teknolojia za kisasa za kilimo, kufadhili miradi inayokabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi na kupanua fursa za kifedha kwa vijana na wanawake ili kuongeza ushiriki wao katika uchumi unaotegemea sekta ya kilimo.

"Tunalenga kuona sekta ya kilimo ikiendelea kuwa injini ya ukuaji wa uchumi wa Taifa kwa kuzalisha ajira, kuongeza kipato cha wananchi na kuiwezesha Tanzania kuwa kitovu cha uzalishaji wa chakula na bidhaa za kilimo katika ukanda wa Afrika," amesema Nyabundege.

Aidha, amesema TADB itaendelea kushirikiana na Serikali, sekta binafsi pamoja na washirika wa maendeleo ili kuongeza rasilimali za uwekezaji na kuimarisha mchango wa sekta ya kilimo katika ukuaji wa uchumi wa nchi.

Sambamba na hilo, ametoa wito kwa wananchi kutembelea banda la TADB katika Maonesho ya 88 ya Kimataifa ya Kilimo (Nane Nane) mwaka 2026 ili kujifunza zaidi kuhusu huduma mbalimbali zinazotolewa na benki hiyo, ikiwemo mikopo, dhamana za kifedha na fursa nyingine zinazolenga kukuza sekta za kilimo, mifugo na uvuvi.







BOHARI ya Dawa (MSD) imeendelea kuthibitisha ubora wake katika usimamizi wa ununuzi wa umma baada ya kutunukiwa Tuzo ya Utendaji Bora katika Ununuzi wa Umma na Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA).

MSD imetambuliwa kama Taasisi Bora kwa Ujumla katika Matumizi ya Mfumo wa Kitaifa wa Ununuzi wa Umma kwa Njia ya Kielektroniki (NeST) kwa mwaka wa fedha 2025/2026, ikiwa ni uthibitisho wa uwazi, ufanisi na matumizi sahihi ya teknolojia katika utekelezaji wa shughuli za ununuzi wa umma.

Tuzo hiyo ilikabidhiwa Julai 29, 2026, wakati wa Kongamano la 10 la Kitaifa la Ununuzi wa Umma, linaloendelea katika Ukumbi wa AICC, Mkoani Arusha.


Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Obedi Laiser (kushoto), akisalimiana na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya TCB, Bw. Adam Mihayo, mara baada ya Bw. Laiser pamoja na ujumbe wake kumtembelea ofisini kwake, jijini Dar es Salaam jana, kwa mazungumzo yenye lengo la kuimarisha mahusiano ya ushirikiano wa kimkakati kati ya taasisi hizo mbili katika kuangalia fursa za kibiashara.

Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Obedi Laiser (kushoto), akimsikiliza Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya TCB, Bw. Adam Mihayo, mara baada ya Bw. Laiser pamoja na ujumbe wake kumtembelea ofisini kwake jijini Dar es Salaam jana, kwa mazungumzo yenye lengo la kuimarisha mahusiano ya ushirikiano wa kimkakati kati ya taasisi hizo mbili katika kuangalia fursa za kibiashara.

Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Obedi Laiser (wa pili kushoto), akizungumza na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya TCB, Bw. Adam Mihayo (kushoto), pamoja na baadhi ya maofisa wa benki hiyo, mara baada ya Bw. Laiser pamoja na ujumbe wake kumtembelea ofisini kwake jijini Dar es Salaam jana, kwa mazungumzo yenye lengo la kuimarisha mahusiano ya ushirikiano wa kimkakati kati ya taasisi hizo mbili katika kuangalia fursa za kibiashara.





Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Obedi Laiser (wa nne kushoto), Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya TCB, Bw. Adam Mihayo (wa tano kushoto), pamoja na baadhi ya maofisa kutoka benki zote mbili, wakipiga picha ya kumbukumbu mara baada ya Bw. Laiser pamoja na ujumbe wake kutembelea ofisini za TCB, jijini Dar es Salaam jana, kwa mazungumzo yenye lengo la kuimarisha mahusiano ya ushirikiano wa kimkakati kati ya taasisi hizo mbili katika kuangalia fursa za kibiashara.


Na. Peter Haule, WF, Arusha

Serikali imesema matumizi ya Mfumo wa Kielektroniki wa Ununuzi wa Umma (NeST) yameendelea kuongezeka nchini, hatua iliyochangia kuimarika kwa uwazi, ushindani, uwajibikaji na matumizi yenye tija ya fedha za umma katika shughuli za ununuzi na ugavi.

Hayo yalielezwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), katika hotuba iliyosomwa kwa niaba yake na Katibu Tawala wa Mkoa wa Arusha, Dkt. Toba Nguvila, wakati wa Kongamano la 10 la Ununuzi wa Umma 2026 lililofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC).

Alisema kuwa hadi Juni 30, 2026, jumla ya wazabuni 45,270 walikuwa wameidhinishwa na kusajiliwa katika Mfumo huo, ambapo asilimia 95 kati yao walikuwa wazabuni wa ndani.

“Katika mwaka wa fedha 2025/2026, hadi Juni 30, 2026, jumla ya tuzo za zabuni 181,057 zenye thamani ya shilingi trilioni 14.5 zilitolewa kupitia mfumo wa NeST, hatua inayoonesha kuongezeka kwa matumizi ya Mfumo huo katika utekelezaji wa shughuli za ununuzi wa umma”, alisema Dkt. Nguvila.

Dkt. Nguvila alisema mafanikio hayo yanaonesha kuwa NeST imeendelea kuwa nyenzo muhimu katika kuimarisha usimamizi wa shughuli za ununuzi wa umma na ugavi, pamoja na kuongeza uwazi, ushindani na thamani ya fedha za umma.

Alisema Mfumo huo pia umeipa Tanzania heshima kimataifa baada ya kuchaguliwa kuwa miongoni mwa Mifumo 20 bora ya Serikali duniani katika Tuzo za World Summit on the Information Society, mafanikio yanayoakisi hatua kubwa iliyopigwa katika mageuzi ya kidijitali kwenye sekta ya ununuzi wa umma na ununuzi endelevu.

Dkt. Nguvila alifafanua kuwa, ujenzi wa Mfumo wa NeST umekamilika kwa asilimia 100 na kwa sasa shughuli zote muhimu za ununuzi wa umma, kuanzia usajili wa wazabuni, uandaaji wa zabuni, usimamizi wa mikataba hadi malipo, zinafanyika kupitia Mfumo huo.

Alisisitiza kuwa taasisi zote za umma zina wajibu wa kutekeleza shughuli za ununuzi kupitia Mfumo wa NeST, akionya kuwa taasisi yoyote itakayofanya ununuzi nje ya Mfumo huo itakuwa imekiuka matakwa ya Sheria ya Ununuzi wa Umma.

"Serikali itaendelea kusimamia matumizi ya Mfumo wa NeST ili kuhakikisha taasisi zote za umma zinafuata sheria na taratibu zilizowekwa," alisema Dkt. Nguvila.

Aidha, Dkt. Nguvila aliipongeza Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA) kwa kuendelea kusimamia utekelezaji wa Sheria ya Ununuzi wa Umma na kuimarisha matumizi ya Mfumo wa NeST, ambapo aliitaka Mamlaka hiyo kuendelea kuuboresha Mfumo huo na kuuunganisha na mifumo mingine ya Serikali ili kuongeza ufanisi, kurahisisha ubadilishanaji wa taarifa na kuimarisha usimamizi wa matumizi ya fedha za umma.

Aliongeza kuwa Serikali inaendelea kutambua ununuzi wa umma kama nyenzo muhimu ya sera ya uchumi inayochochea maendeleo ya viwanda vya ndani, kukuza ushiriki wa wazabuni wazawa, kuongeza ajira na kuchangia ukuaji wa uchumi wa Taifa pamoja na kufanikisha malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA), Bw. Dennis Simba, alisema taasisi zote za Serikali zinapaswa kuzingatia kikamilifu Sheria ya Ununuzi wa Umma, akisisitiza kuwa taasisi zitakazoshindwa kutekeleza matakwa ya sheria hiyo zitawekwa hadharani, ikiwa ni utekelezaji wa maelekezo ya, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Bw. Simba pia aliwapongeza wadau walioshiriki Kongamano la 10 la Ununuzi wa Umma 2026 na kuwataka kutumia fursa hiyo kuongeza uelewa na uwezo wa kitaalamu ili kuendelea kuboresha utekelezaji wa shughuli za ununuzi wa umma nchini.

Katibu Tawala Mkoa wa Arusha, Dkt. Toba Nguvila (kushoto), akipata maelezo kuhusu Sera ya Ununuzi wa Umma, kutoka kwa Afisa Ugavi Mwandamizi Idara ya Sera za Ununuzi wa Umma Wizara ya Fedha, Bw. Richard Benaya, alipotembelea Banda la Wizara ya Fedha wakati wa Kongamano la 10 la Ununuzi wa Umma 2026, linalofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC). Kushoto ni Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA), Bw. Dennis Simba

Katibu Tawala Mkoa wa Arusha, Dkt. Toba Nguvila (kushoto), akiagana na  Afisa Ugavi Mwandamizi Idara ya Sera za Ununuzi wa Umma Wizara ya Fedha, Bw. Richard Benaya, baada ya kutembelea Banda la Wizara ya Fedha wakati wa Kongamano la 10 la Ununuzi wa Umma 2026, linalofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC).

Katibu Tawala Mkoa wa Arusha, Dkt. Toba Nguvila, akiitaka Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA) kuhakikisha Mfumo wa Kielektroniki wa Ununuzi wa Umma (NeST) unasomana na Mifumo mingine Serikalini ili kurahisisha utendaji, wakati wa Kongamano la 10 la Ununuzi wa Umma 2026, linalofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC).

Kamishana Idara ya Sera za Ununuzi wa Umma Bw. Alex Haraba, akifuatilia maelezo ya Katibu Tawala Mkoa wa Arusha, Dkt. Toba Nguvila, wakati wa Kongamano la 10 la Ununuzi wa Umma 2026, linalofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC).

Mkurugenzi wa Kitengo cha Ununuzi, Wizara ya Fedha, Bw. Boaz Ntembanda akifuatilia maelezo ya Katibu Tawala Mkoa wa Arusha, Dkt. Toba Nguvila, wakati wa Kongamano la 10 la Ununuzi wa Umma 2026, linalofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC).


Afisa Ugavi Mwandamizi Idara ya Sera za Ununuzi wa Umma, Wizara ya Fedha, Bi. Jamila Byekwaso, akitoa elimumu ya Sera  za Ununuzi wa Umma, kwa wadau wa Kongamano la 10 la Ununuzi wa Umma 2026, linalofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC).

Baadhi ya Maafisa wa Idara ya Sera za Ununuzi wa Umma, Wizara ya Fedha, wakiwa katika picha ya pamoja wakati wa Kongamano la 10 la Ununuzi wa Umma 2026, linalofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC).

Kongamano la 10 la Ununuzi wa Umma 2026, linalofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC).

 

 (Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Fedha, Arusha)


Na. Ramadhani Kissimba, Durban.


Nchi wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) zimeshauriwa kuwekeza zaidi katika maendeleo ya viwanda na miundombinu ili kuwawezesha wanawake na vijana kushiriki kikamilifu katika shughuli za uzalishaji na kuongeza mchango wao katika ukuaji wa uchumi wa ukanda wa SADC.

Ushauri huo umetolewa jijini Durban nchini Afrika Kusini na Meneja wa Utafiti na Biashara wa Benki ya Maendeleo Tanzania (TIB), Dkt. Hilderbrand Shayo, kando ya Mkutano wa Wiki ya Viwanda wa SADC unaoendelea nchini humo.

Alisema kuwa uwekezaji katika viwanda vya kuongeza thamani ya bidhaa utasaidia kuwainua wanawake na vijana kiuchumi, kupanua masoko ya bidhaa za Tanzania na kuongeza mapato yatokanayo na mauzo ya bidhaa nje ya nchi.

Akizungumzia kuhusu ushiriki wa Tanzania katika mkutano na maonesho hayo, Dkt. Shayo alisema matukio hayo yanaendana na vipaumbele vya maendeleo vya Tanzania, hususan katika sekta za madini, kilimo, bidhaa za afya pamoja na maendeleo ya miundombinu na ubunifu, ambazo ni maeneo yanayopewa kipaumbele katika kufikia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

"Ushiriki wa Tanzania katika Wiki ya Viwanda ya SADC una umuhimu mkubwa kwa sababu mkutano huu umejikita katika kuimarisha mnyororo wa thamani wa sekta za madini, kilimo na bidhaa za afya, sambamba na maendeleo ya miundombinu na ubunifu na ni maeneo muhimu katika safari ya Tanzania kuelekea uchumi wa viwanda na maendeleo endelevu," alisema Dkt. Shayo.

Aidha, alisema kuwa maonesho hayo yamefungua fursa mpya za uwekezaji, ambapo wawekezaji kutoka nchi mbalimbali wameonesha nia ya kuwekeza nchini Tanzania kutokana na mazingira mazuri ya biashara pamoja na nafasi ya kimkakati ya nchi hiyo kama lango la biashara kupitia Bandari ya Dar es Salaam inayohudumia nchi nyingi wanachama wa SADC.

Dkt. Shayo, aliongeza kuwa ushiriki wa Tanzania katika maonesho hayo umeiwezesha nchi kuzitangaza fursa zake za uwekezaji na kuimarisha ushirikiano wa kibiashara na wadau mbalimbali wa maendeleo kutoka ndani na nje ya ukanda wa SADC.

Sambamba na hilo, Dkt. Shayo alizishauri taasisi za fedha zilizoshiriki katika mkutano huo, ikiwemo Benki ya Maendeleo Tanzania (TIB), Benki ya Exim, BADEA, Nedbank na taasisi nyingine za kifedha, kuimarisha ushirikiano katika kutafuta mitaji na fedha za kugharamia miradi ya maendeleo na uwekezaji nchini Tanzania.

"Taasisi za fedha zilizoshiriki katika maonesho haya zina nafasi kubwa ya kushirikiana katika kuhamasisha upatikanaji wa fedha kwa ajili ya miradi ya maendeleo na uwekezaji ambayo itachochea ukuaji wa uchumi wa Tanzania," alisema Dkt. Shayo

Akizungumzia sekta ya madini, Dkt. Shayo alisema Tanzania imebarikiwa kuwa na madini mengi ya kimkakati yanayohitajika duniani, hususan katika kipindi hiki cha maendeleo ya teknolojia.

Alisisitiza umuhimu wa kuyachakata madini hayo ndani ya nchi badala ya kuuza malighafi pekee, hatua ambayo itaongeza thamani ya bidhaa, kuzalisha ajira zaidi, kuongeza mapato ya fedha za kigeni na kuchochea ukuaji wa viwanda vya ndani.

Mkutano wa Wiki ya Viwanda wa SADC umeendelea kuwa jukwaa muhimu la kuimarisha ushirikiano wa kikanda katika biashara, uwekezaji na maendeleo ya viwanda. Kwa Tanzania, ushiriki katika mkutano huo unaendelea kufungua fursa mpya za uwekezaji, masoko na ubia wa kifedha, huku ukiunga mkono juhudi za Serikali za kujenga uchumi wa viwanda, kuongeza thamani ya rasilimali za ndani na kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.


Baadhi ya Washiriki wa Wiki ya Tisa ya Viwanda kutoka nchi wanachama wa SADC wakifuatilia mojawapo ya mjadala kuhusu masuala ya madini uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano (ICC), Durban, Afrika Kusini.

Meneja wa Mawasiliano, Masoko na Mahusiano wa Benki ya Maendeleo - TIB, Bw. Allan Chonjo akitoa maelezo kuhusu bidhaa na huduma zinazotolewa na Benki hiyo kwa baadhi ya wadau waliotembelea Banda la Tanzania, pembezoni mwa Mkutano wa Wiki ya Viwanda ya SADC (SADC Industrialisation Week 2026) unaofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano (ICC), jijini Durban, Afrika Kusini.

Afisa Sheria kutoka Tume ya Ushindani (FCC) akielezea ubora na faida za mkonge unaozalishwa Tanzania kwa mdau aliotembelea Banda la Tanzania, pembezoni mwa Mkutano wa Wiki ya Viwanda ya SADC (SADC Industrialisation Week 2026) unaofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano (ICC), jijini Durban, Afrika Kusini.

Baadhi ya Washiriki kutoka Wizara na Taasisi mbalimbali wakiwa katika picha ya Pamoja baada ya Mkutano wa Wiki ya Viwanda ya SADC (SADC Industrialisation Week 2026) unaofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano (ICC), jijini Durban, Afrika Kusini.


Katika kuendeleza dhamira yake ya kuchangia maendeleo ya jamii kupitia mpango wa Uwajibikaji kwa Jamii (CSI) chini ya kampeni yake ya #PSSSFKaribuNaJamii, Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) umekabidhi rasmi mradi wa miundombinu wenye thamani ya Shilingi milioni 25 katika Shule ya Msingi Majani Mapana iliyopo mkoani Tanga.

Mradi huo unahusisha ujenzi wa chumba cha darasa, chumba cha mapumziko pamoja na vifaa mbalimbali vya michezo kwa ajili ya watoto wenye mahitaji maalum.

Akizungumza wakati wa makabidhiano hayo, Bw. Kwame Temu alieleza kuwa msaada huo unalenga kuunga mkono juhudi za Serikali kwa kuhakikisha watoto wenye mahitaji maalum wanapata haki yao ya msingi ya elimu. Alisisitiza kuwa hatua hiyo itawasaidia wanafunzi hao kujifunza katika mazingira yanayowawezesha kujifunza kwa ufanisi, kushiriki katika michezo na kukuza vipaji vyao mbalimbali.

Kwa upande wake, Afisa Elimu Kata ya Nguvumali, Bi. Lilian Shetui, aliishukuru PSSSF kwa mchango huo akieleza kuwa miundombinu hiyo itaongeza ubora wa huduma za elimu shuleni hapo. Kwa niaba ya Afisa Elimu Shule za Awali na Msingi wa mkoa huo, Bi. Lilian alipongeza PSSSF kwa kuona umuhimu wa kundi hilo na kutoa msaada utakaokuwa na tija kubwa kwa watoto hao.

Kupitia mchango huo, jumla ya wanafunzi 71 wenye mahitaji maalum na usonji katika Shule ya Majani Mapana wanatarajiwa kunufaika na mazingira rafiki ya kujifunzia, kupumzika na kucheza, hatua inayochochea elimu jumuishi na kuwajengea msingi bora wa maisha ya baadaye.




Top News