Na Mwandishi Wetu

SERIKALI  imeombwa kuzipa nafasi kampuni zenye uwezo wa kuzalisha gesi ya Okseji ambayo inajukulikana kwa jina la hewa tiba kwa  ajili ya matumizi ya hospitalini kwa kuwa kampuni hizo zinauwezo mkubwa na zimebobea katika uzalishaji huo.

Ombi hilo limetolewa leo jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya TOL Gases PLC Daniel Warungu alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari baada ya kumalizika kwa Mkutano Mkuu wa 31 wa mwaka wa Wanahisa huku akisisitiza wao wamekuwa na uwezo mkubwa wa kuzalisha.

Amesema kwa sekta binafsi zinazalisha gesi ya Oksijeni hivyo ni vema Serikali ikawa inanunua badala ya kuzalisha na kupikia mitambo huku akifafanua anaamini serikali itakubali ombi hilo kwa kuwa imeonesha nia huku akisisitiza uwepo wa nyenzo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 imeonesha jinsi ambavyo sekta binafsi zinavyoweza kuwa mshirika katika utekelezaji wa dira na wao TOL Gases wako tayari.

“Tunafanya uwekezaji mkubwa unaowezesha kuzalisha gesi ya oksijeni kwa ajili ya kuhakikisha kunakuwa na hewa tiba kwa ajili ya mahospitalini hivyo ombi letu Serikali badala ya nayo kuwa inazalisha iweke utaratibu wa kuwa inanunua kutoka sekta binafsi.TOL Gases tunao uwezo mkubwa na tumebobea katika uzalishaji wa oksijeni.”

Kuhusu mkutano wa wanahisa Warungu amesema wamejadili masuala mbalimbali huku akieleza kwa upande wa mapato ya kampuni yaliongezeka kutoka Shilingi bilioni 30.2 mwaka 2024 hadi Shilingi bilioni 31.15 mwaka 2025. 

Amefafanua faida kabla ya riba, kodi, uchakavu na punguzo la thamani (EBITDA) iliongezeka kutoka Shilingi bilioni 10.5 hadi Shilingi bilioni 13.4, huku faida kabla ya kodi ikiongezeka kutoka Shilingi bilioni 3.98 hadi Shilingi bilioni 6.78.”Faida baada ya kodi ilifikia Shilingi bilioni 3.98 mwaka 2025, ikilinganishwa na Shilingi bilioni 2.06 mwaka 2024.”

Ameongeza TOL Gases inaendelea kuongeza uwezo wake wa uzalishaji kupitia miradi miwili mikubwa. Miongoni mwa miradi hiyo ni ujenzi wa kiwanda cha Ikama III cha kuzalisha hewa ya ukaa (Carbon Dioxide), kinachotarajiwa kuanza uzalishaji Septemba 2027. Mradi huo utaongeza uwezo wa uzalishaji na kuimarisha upatikanaji wa gesi hiyo.

Aidha kampuni pia inajenga kituo kipya cha kutenganisha hewa (Air Separation Unit – ASU) kwa msaada wa Clinton Health Access Initiative (CHAI). Kituo hicho kinatarajiwa kuanza kufanya kazi Oktoba 2026 na kitaongeza uwezo wa uzalishaji wa oksijeni hadi takribani tani 20 kwa siku, sambamba na kituo kilichoanza kufanya kazi mwaka 2021.

Warungu amesisitiza uwekezaji huo utasaidia kuongeza ufanisi wa uzalishaji, kurahisisha matengenezo ya mitambo bila kuathiri kwa kiasi kikubwa uzalishaji na kuongeza uwezo wa kukidhi mahitaji ya gesi katika sekta ya afya, viwanda na uzalishaji.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Kampuni hiyo Leonard Kitoka amesema Tanzania kwa sasa ina uwezo wa kutosha kutoka kwa wazalishaji binafsi kukidhi mahitaji ya sasa na yajayo ya oksijeni ya tiba, hasa kutokana na uwekezaji mkubwa uliofanywa hivi karibuni katika mitambo ya uzalishaji.

Akizungumza kuhusu Soko la hisa,amesema  thamani ya hisa za TOL Gases katika Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE) imeongezeka kutoka Shilingi 795 wakati wa Mkutano Mkuu wa Mwaka uliopita hadi kufikia kiwango cha juu cha Shilingi 1,490, sawa na ongezeko la takribani asilimia 74. Kwa sasa, hisa hizo zinauzwa kati ya Shilingi 1,320 na Shilingi 1,490.

“TOL Gases imeeleza kuwa rasilimali za umma zinaweza kutumika kwa ufanisi zaidi katika kuongeza mahitaji na upatikanaji wa oksijeni ya tiba badala ya kuwekeza katika kuongeza zaidi uwezo wa uzalishaji.

“Kampuni inapendekeza hospitali na vituo vya afya kuwezeshwa kununua oksijeni yenye ubora unaohakikishwa kutoka kwa wazalishaji binafsi waliopo, hatua ambayo kwa mujibu wa kampuni itasaidia kutumia kikamilifu uwezo wa uzalishaji uliopo nchini, kuepusha uwekezaji unaojirudia na kuhakikisha upatikanaji endelevu wa oksijeni kwa gharama nafuu.”

Amesisitiza TOL Gases  itaendelea kushirikiana na Serikali, taasisi za afya na wadau wa maendeleo kuhakikisha upatikanaji wa oksijeni salama na yenye ubora kwa matumizi ya tiba nchini Tanzania, huku ikiendelea kuwekeza katika uzalishaji, usambazaji na utaalamu wa kiufundi.

Pamoja na hayo amesema kutokana na mikakati ya kampuni hiyo wanahisa kwa kauli moja wamekubaliana kutogawana gawio la faida na badala yake fedha hizo za gawio zitumike katika kuwekeza katika Ujenzi wa miundombinu kwanza ili kuongeza mapato ya kampuni.







Na Mwandishi Wetu

MAMLAKA ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) imeteketeza hekari 3,117.9 za mashamba ya bangi na kukamata watuhumiwa 12 katika operesheni maalum ya siku 16 iliyofanyika katika vijiji vinne vya Kata ya Kandawale na Kipatimo, Wilaya ya Kilwa, mkoani Lindi.

Akizungumza kuhusu operesheni hiyo, Kamishna Jenerali wa DCEA, Aretas Lyimo, amesema mafanikio hayo yametokana na ushirikiano mkubwa kati ya Mamlaka, wananchi na viongozi wa maeneo husika katika mapambano dhidi ya kilimo cha bangi.

Amesema operesheni hiyo ni sehemu ya mkakati endelevu wa DCEA wa kudhibiti uzalishaji wa dawa za kulevya nchini hususan bangi, ambayo imeendelea kulimwa katika baadhi ya maeneo nchini.

"Tumebaini uwepo wa mashamba makubwa ya bangi yaliyolimwa katika ardhi zinazomilikiwa na vijiji na vitongoji. Licha ya serikali kuweka mkakati wa matumizi ya ardhi iliyopo chini ya vijiji na vitongoji lakini bado wananchi wanaitumia ardhi hiyo kulima bangi" amesema Lyimo.

Ameeleza kuwa, kati ya wananchi 200 hadi 250 walishiriki kila siku katika kufyeka mashamba hayo, jambo linalodhihirisha umuhimu wa ushiriki wa jamii katika mapambano dhidi ya dawa za kulevya.

Aidha, ametoa wito kwa wananchi wote wenye mashamba ya bangi au wanaofahamu uwepo wa mashamba hayo katika maeneo yao nchini kuyateketeza mara moja kabla ya hatua za kisheria kuchukuliwa. Vilevile, amewataka viongozi wa vijiji na kata kuhakikisha wanazuia na kutokomeza kilimo cha bangi katika maeneo yao.

Vilevile, amewataka wasimamizi wa hifadhi za taifa na maeneo mengine ya uhifadhi kuhakikisha maeneo wanayosimamia hayatumiki kulima bangi, akisisitiza kuwa hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi ya yeyote atakayebainika kuruhusu au kushindwa kudhibiti shughuli hizo.

Kwa upande wao, wananchi wa Kijiji cha Nandete, Veronica Mandai na Nassoro Mbonde, wamelaani vikali uwepo wa kilimo cha bangi katika maeneo yao, wakisema kuwa hakina manufaa kwa jamii na kimekuwa kikihatarisha mustakabali wa vijana.

Wamesema wakati mwingine watoto wao hujihusisha na kilimo hicho bila wazazi kufahamu, ndiyo sababu wamejitokeza kwa wingi kushiriki katika zoezi la kuteketeza mashamba ya bangi ili kuonyesha msimamo wao wa kupinga kilimo hicho.

"Nawaomba vijana na wanawake wawe mstari wa mbele kukataa na kutokomeza dawa za kulevya kwa sababu zina madhara makubwa kwa afya na maendeleo ya jamii. Vijana ndiyo nguvu kazi ya taifa na wanawajibu wa kulijenga Taifa. Wakijiingiza katika matumizi au uzalishaji wa dawa za kulevya, watapoteza fursa hiyo na kuathiri maendeleo ya taifa. Vilevile, watoto wanaokulia katika mazingira yanayohusisha dawa za kulevya wako katika hatari ya kupoteza mwelekeo wa maisha yao," amesema Veronica.

Naye Afisa Mtendaji wa Kata ya Kandawale, Mohamed Mpame, amesema baada ya operesheni hiyo viongozi wa kata kwa kushirikiana na vijiji na vitongoji wataimarisha ulinzi na usimamizi wa maeneo yao ili kuhakikisha kilimo cha bangi hakiendelei.

"Tutahakikisha tunafanya doria za mara kwa mara na kuendelea kutoa elimu kwa wananchi ili waachane kabisa na kilimo cha bangi ili mwisho wa siku likitokea la kutokea iwe ni juu yao. Nawashauri watu kutumia ardhi yao kulima mazao ya korosho na kuachana na mazao ya bangi” amesema Mpame.

DCEA itaendelea kufanya operesheni nchi nzima kwa kushirikiana na wananchi na wadau mbalimbali ili kubaini na kutokomeza maeneo yote yanayotumika kwa kilimo cha bangi na kuhakikisha hatua stahiki zinachukuliwa kwa mujibu wa sheria.








 

NAIBU Waziri wa Viwanda na Biashara, Dennis Londo,akizungumza wakati wa Mkutano wa Kati ya Wizara na Wakuu wa Sehemu na Idara za Viwanda,Biashara na Uwekezaji katika Sekretariet za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kinachofanyika kuanzia leo Agosti 17 hadi 18 jijini Dodoma.

NAIBU Waziri wa Viwanda na Biashara, Dennis Londo,akizungumza wakati wa Mkutano wa Kati ya Wizara na Wakuu wa Sehemu na Idara za Viwanda,Biashara na Uwekezaji katika Sekretariet za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kinachofanyika kuanzia leo Agosti 17 hadi 18 jijini Dodoma.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara, Balozi Waziri Salum,akizungumza wakati wa Mkutano wa Kati ya Wizara ya Viwanda na Biashara na Wakuu wa Sehemu na Idara za Viwanda,Biashara na Uwekezaji katika Sekretariet za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kinachofanyika kuanzia leo Agosti 17 hadi 18 jijini Dodoma.

 Afisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA), Godfrey Nyaisa,akizungumza wakati wa Mkutano wa Kati ya Wizara ya Viwanda na Biashara na Wakuu wa Sehemu na Idara za Viwanda,Biashara na Uwekezaji katika Sekretariet za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kinachofanyika kuanzia leo Agosti 17 hadi 18 jijini Dodoma.

SEHEMU ya washiriki wakimsikiliza Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Dennis Londo (hayupo pichani) ,akizungumza wakati wa Mkutano wa Kati ya Wizara na Wakuu wa Sehemu na Idara za Viwanda,Biashara na Uwekezaji katika Sekretariet za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kinachofanyika kuanzia leo Agosti 17 hadi 18 jijini Dodoma.

SEHEMU ya washiriki wakimsikiliza Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Dennis Londo (hayupo pichani) ,akizungumza wakati wa Mkutano wa Kati ya Wizara na Wakuu wa Sehemu na Idara za Viwanda,Biashara na Uwekezaji katika Sekretariet za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kinachofanyika kuanzia leo Agosti 17 hadi 18 jijini Dodoma.

NAIBU Waziri wa Viwanda na Biashara, Dennis Londo,akiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kugungua Mkutano wa Kati ya Wizara na Wakuu wa Sehemu na Idara za Viwanda,Biashara na Uwekezaji katika Sekretariet za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kinachofanyika kuanzia leo Agosti 17 hadi 18 jijini Dodoma.

NAIBU Waziri wa Viwanda na Biashara, Dennis Londo,akiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kugungua Mkutano wa Kati ya Wizara na Wakuu wa Sehemu na Idara za Viwanda,Biashara na Uwekezaji katika Sekretariet za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kinachofanyika kuanzia leo Agosti 17 hadi 18 jijini Dodoma.

NAIBU Waziri wa Viwanda na Biashara, Dennis Londo,akiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kugungua Mkutano wa Kati ya Wizara na Wakuu wa Sehemu na Idara za Viwanda,Biashara na Uwekezaji katika Sekretariet za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kinachofanyika kuanzia leo Agosti 17 hadi 18 jijini Dodoma.

............

NAIBU Waziri wa Viwanda na Biashara, Dennis Londo, amewataka Maafisa Biashara nchini kutumia nafasi zao kikamilifu kuibua fursa za uwekezaji, kuongeza thamani ya mazao na kuboresha mazingira ya biashara katika halmashauri, hatua inayolenga kuchochea maendeleo ya kiuchumi na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Londo ametoa kauli hiyo leo Agosti 17,2026 jijini Dodoma  wakati wa Kikao cha Tatu cha Wizara ya Viwanda na Biashara na Maafisa Biashara nchini, kilicholenga kuimarisha utekelezaji wa majukumu yao katika kukuza biashara, viwanda na uwekezaji.

Amesema Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inalenga kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha uchumi wa viwanda katika Afrika Mashariki na Kati, ikiwamo kufikia uchumi wa dola trilioni moja na kuongeza kipato cha Mtanzania hadi dola 7,000. Amesema kufikia malengo hayo kunahitaji uchumi imara, jumuishi na shindani unaotegemea sekta binafsi, sayansi na teknolojia, uwekezaji, utafiti pamoja na nguvu kazi yenye ujuzi.

"Maafisa Biashara wana jukumu la kuhakikisha halmashauri zinakuwa vituo vya uzalishaji, uwekezaji na biashara kwa kutambua fursa zilizopo, kuwaunganisha wazalishaji na masoko na kuhakikisha mazao yanaongezwa thamani. "amesema Mhe.Londo

Hata hivyo ametolea mfano wa mahindi, amesema wakulima wanapaswa kusaidiwa kuondokana na kuuza mazao ghafi na badala yake kuzalisha bidhaa kama unga wenye chapa na kuufikisha kwenye masoko, hatua itakayoongeza kipato na kuchangia kupunguza umaskini.

Aidha, amesema utekelezaji wa Dira 2050 unahitaji vijana, wanawake na watu wenye ulemavu kushirikishwa kikamilifu katika uzalishaji, uwekezaji na biashara kupitia fursa za mikopo na uwezeshaji. Amesema katika mwaka wa fedha 2025/2026, viwanda vikubwa vipya 25 vilijengwa katika sekta mbalimbali na kutoa ajira 39,000, zikiwamo ajira 7,600 za moja kwa moja na 31,000 zisizo za moja kwa moja.

Katika kuimarisha mazingira ya uwekezaji, Londo amezitaka mikoa kuhuisha kanzidata za viwanda, biashara, masoko, leseni, wawekezaji na maeneo yaliyotengwa kwa shughuli za kiuchumi, huku kila halmashauri ikiandaa wasifu wa fursa za uwekezaji unaoonyesha upatikanaji wa malighafi, miundombinu, masoko na maeneo ya uwekezaji. Pia amewataka Maafisa Biashara kuhakikisha Mabaraza ya Biashara yanafanya kazi kikamilifu na hoja za sekta binafsi zinapatiwa ufumbuzi kwa wakati.

Katika hatua nyingine, Londo amewataka Maafisa Biashara kuharakisha urasimishaji wa biashara zisizo rasmi kwa kutoa elimu kuhusu usajili wa biashara, leseni, TIN, viwango, vipimo na taarifa za umiliki.

Amesema urasimishaji utawawezesha wafanyabiashara kupata huduma za uwezeshaji, mitaji na masoko, huku akieleza kuwa halmashauri zimetengewa asilimia tano ya mapato ya ndani, yenye thamani ya zaidi ya Sh bilioni 72 kwa mwaka wa fedha 2026/2027, kwa ajili ya kuwekeza katika miundombinu ya masoko, maeneo ya biashara na ujasiriamali.

Amesisitiza fedha hizo zitumike kwa ufanisi kwa kushirikisha sekta za ardhi, maji, nishati na barabara ili kuongeza tija kwa wafanyabiashara na kuvutia wawekezaji. Aidha, amewataka Maafisa Biashara kutumia nafasi zao kuboresha huduma na kuifanya Tanzania kuwa na mazingira bora zaidi ya biashara na uwekezaji, hatua ambayo ni muhimu katika kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara, Balozi Waziri Salum, amewataka Maafisa Biashara kuongeza udhibiti wa bidhaa feki na viwanda visivyo rasmi katika maeneo yao, akieleza kuwa hatua hiyo ni muhimu katika kulinda afya na usalama wa wananchi, watumiaji pamoja na wazalishaji wanaofuata sheria.

Naye Afisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA), Godfrey Nyaisa, amesema Maafisa Biashara ni kiungo muhimu kati ya Serikali na wafanyabiashara katika kuhakikisha sera, sheria na kanuni za biashara zinatekelezwa na kuleta mabadiliko chanya katika mazingira ya biashara na uwekezaji nchini.

Amesema kuelekea utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, BRELA imeendelea kuboresha mifumo na sheria zinazosimamia usajili na utoaji wa leseni kwa lengo la kupunguza muda na gharama za kuanzisha na kuendesha biashara. Amesema kupitia BRELA Online System (ORS), huduma za wakala zimeunganishwa katika mfumo mmoja, huku mfumo huo ukiwezesha pia utoaji na usimamizi wa leseni za biashara kundi A na B.

Amesema mfumo huo unatoa fursa kwa Mamlaka za Serikali za Mitaa kutoa na kusimamia leseni za kundi B bila kuathiri mapato yao, kwani malipo yanayofanywa na mfanyabiashara yanaingia moja kwa moja katika akaunti ya halmashauri husika.

Aidha, ORS imeunganishwa na mifumo ya taasisi nyingine za Serikali ikiwamo NIDA na TRA, hatua inayowezesha taarifa muhimu kupatikana moja kwa moja bila mfanyabiashara kuwasilisha nyaraka ambazo tayari zipo kwenye mifumo hiyo.

Nyaisa,amesema kuwa  maboresho hayo yameongeza uwazi na ufanisi, kupunguza urudufu wa taarifa, muda na gharama za kupata huduma, pamoja na kupunguza mianya ya uzembe katika utoaji wa huduma.

"BRELA itaendelea kushirikiana na Wizara ya Viwanda na Biashara, Ofisi ya Waziri Mkuu–TAMISEMI, sekretarieti za mikoa na halmashauri katika kuwajengea uwezo Maafisa Biashara."amesema Nyaisa

Amesema katika mwaka wa fedha 2026/2027, BRELA imepanga kutoa mafunzo kwa Maafisa Biashara wote nchini kupitia kanda nne, yatakayolenga matumizi ya mifumo, utoaji na usimamizi wa leseni pamoja na utekelezaji wa sheria.

Pia amesema BRELA itaendelea kuboresha miunganiko ya mifumo ya kidijitali na kushirikiana na vyama vya Maafisa Biashara katika kutatua changamoto zao, huku akisisitiza kuwa maafisa hao ni mawakala muhimu wa uwekezaji nchini na wanapaswa kutambua kuwa jukumu lao ni kuwezesha biashara, si kuikwamisha, ili kujenga mazingira rafiki kwa wafanyabiashara na wawekezaji.

Na. Mwandishi Wetu - Nzega

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Prof. Palamagamba Kabudi, leo Agosti 17, 2026, ametembelea, kukagua na kukabidhi miradi inayotekelezwa kupitia Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (Agriculture and Fisheries Development Programme – AFDP) katika Shamba la Mbegu la Wakala wa Mbegu Tanzania (ASA), Kilimi, Wilaya ya Nzega, Mkoa wa Tabora.

Programu hiyo inafadhiliwa na Shirika la Kimataifa la Maendeleo ya Kilimo (IFAD), ikiwa na lengo la kuongeza tija, kuimarisha uzalishaji wa mbegu bora na kuchochea maendeleo ya sekta ya kilimo nchini.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Prof. Kabudi amesema sekta ya kilimo ni mhimili muhimu wa ukuaji wa uchumi wa Tanzania kutokana na mchango wake katika pato la Taifa, usalama wa chakula, ajira na biashara ya nje.

“Programu hii ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi ni muhimu kwa sekta ya kilimo kwa kuwa inalenga kuongeza tija katika sekta ya kilimo ambayo ni mhimili wa maendeleo ya uchumi. Sekta hii inachangia kiasi cha nusu ya pato la Taifa, robo tatu ya bidhaa zinazouzwa nje ya nchi na ni chanzo cha chakula pamoja na kutoa fursa za ajira kwa zaidi ya asilimia 75 ya Watanzania,” amesema Prof. Kabudi.

Aidha, Waziri Kabudi amekabidhi rasmi jengo la ofisi, jengo la karakana na jengo la kukaushia mbegu kwa Wizara ya Kilimo, miradi ambayo imetekelezwa kupitia Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) kwa ufadhili wa IFAD.

Kabla ya kukabidhi miradi hiyo, Prof. Kabudi alikagua miradi mbalimbali inayotekelezwa katika Shamba la Mbegu la Kilimi, ikiwemo ujenzi wa karakana, eneo la kukaushia mazao (drying shade), ofisi na ukumbi wa mafunzo pamoja na nyumba mbili za watumishi.

Vilevile, programu hiyo imewezesha upatikanaji wa zana na vifaa vya kisasa vya kilimo, ikiwemo boom sprayer, disc harrow, matrekta, maize sheller, tiller, vifaa vya karakana pamoja na magari kwa ajili ya usimamizi na usambazaji wa mbegu.

Akihitimisha ziara hiyo, Prof. Kabudi amesisitiza umuhimu wa utekelezaji wa miradi kwa wakati, kwa kuzingatia viwango na ubora uliokusudiwa ili kuhakikisha thamani halisi ya fedha iliyowekezwa (value for money) inapatikana.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa kuwa na mpango mkakati madhubuti wa utekelezaji ili kuhakikisha malengo ya Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi yanafikiwa ndani ya muda uliopangwa.

Katika ziara hiyo, Waziri Kabudi ameambatana na Naibu Waziri wa Kilimo, Mhe. David Silinde, Naibu Katibu Mkuu anayeshughulikia Umwagiliaji na Zana za Kilimo, Mhandisi Athumani Kilundumya, Mkurugenzi wa Sera na Uratibu kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, Bw. Paul Sangawe, pamoja na Mratibu wa Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, Bw. Salum Mwinjaka.













Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Kimataifa la Uhamiaji (IOM) Bi. Amy E. Pope, tarehe 17 Agosti,2026 Ikulu Ndogo, Zanzibar.
02: Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Kimataifa la Uhamiaji (IOM) Bi. Amy E. Pope, tarehe 17 Agosti,2026 Ikulu Ndogo, Zanzibar.



Na Janeth Raphael - MichuziTv

Upande wa Jamhuri umefunga ushahidi wake baada ya kuwasilisha ushahidi wa mashahidi 17 katika kesi ya uhaini inayomkabili Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Tundu Lissu.

Hatua hiyo imefikiwa leo Jumatatu, Agosti 17, 2026, katika Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo, Dar es Salaam, wakati kesi hiyo ikiendelea kusikilizwa mbele ya jopo la majaji watatu.

Wakili wa Serikali Mkuu, Nassoro Katuga, ameieleza Mahakama kuwa baada ya upande wa Jamhuri kupitia kwa kina ushahidi uliotolewa na mashahidi wake pamoja na hoja mbalimbali zilizowasilishwa wakati wa usikilizwaji wa kesi, umefikia uamuzi kuwa ushahidi uliopo unatosheleza.

Kwa mujibu wa Katuga, uchambuzi wa ushahidi uliowasilishwa mahakamani umeifanya Jamhuri kuona hakuna ulazima wa kuongeza mashahidi wengine, hivyo upande huo umefunga rasmi ushahidi wake.

“Baada ya kupitia ushahidi uliowasilishwa hapa mahakamani na kuangalia ushahidi wa mashahidi waliobakia, tumechambua na kuangalia hoja zilizowasilishwa mahakamani hapa. Hata hivyo, upande wa Jamhuri tunaona ushahidi ambao tumeutoa ni ushahidi toshelezi zaidi kuleta mashahidi wengine,” amesema Katuga.

Uamuzi huo unaweka kesi hiyo katika hatua muhimu, baada ya upande wa mashtaka kukamilisha uwasilishaji wa ushahidi wake kupitia mashahidi 17.

Kesi hiyo inasikilizwa na jopo la majaji watatu likiongozwa na Jaji Dunstan Ndunguru, akisaidiwa na Jaji James Karayemaha na Jaji Ferdinand Kiwonde.

Kufungwa kwa ushahidi wa Jamhuri kunafungua hatua nyingine ya kisheria katika mwenendo wa kesi hiyo, huku taratibu za mahakama zikiendelea kuamua hatua zinazofuata.






MAONESHO ya uchumi bunifu yanayoenda kwa jina la Mashariki Creative Economy Expo 2026 yanaanza  jijini Dar es Salaam kuanzia kesho tarehe 18 hadi 21 Agosti 2026, yakiwakutanisha wabunifu, wawekezaji, watangazaji, wamiliki wa haki, watunga sera na wabunifu wa teknolojia kwa ajili ya kukuza uchumi wa ubunifu barani Afrika.

Maonesho hayo yaliyoandaliwa na taasisi isiyo ya kiserikali ya  Culture and Development East Africa (CDEA) yanalenga kuifanya sekta ya ubunifu kuwa chanzo cha fursa za biashara na uwekezaji, kupitia matumizi ya haki miliki (IP) katika muziki, filamu, fasihi, sanaa za picha, maudhui ya kidijitali na maeneo mengine.

Expo hiyo pia inalenga kujenga ushirikiano wa kimkakati na majukwaa ya habari na burudani kama Azam Max, ili kukuza simulizi za Afrika Mashariki, kuibua vipaji vipya na kuunganisha wabunifu na masoko mapana ya kikanda na kimataifa.

#MasharikiExpo2026 #UchumiWaUbunifu #CDEA #VipajiAfrika #HakiMiliki #DarEsSalaam #AfrikaMashariki



Na Mwandishi Wetu
WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais (Mipango na Uwekezaji), Profesa Kitila Mkumbo, amepongeza ubunifu ulioonyeshwa na wanafunzi wa Chuo cha St Joseph jijini Dar es Salaam, akisema ukiendelezwa unaweza kutatua changamoto nyingi zinazoikabili jamii.

Amesema Serikali itashirikiana na vyuo binafsi kuhakikisha masomo ya sayansi yanapewa kipaumbele ili kupatikane wahandisi wengi nchini na kuondoa utegemezi wa wataalamu wa kigeni. Aliyasema hayo mwishoni mwa wiki wakati akizungumza kwenye Wiki ya Tafiti na Ubunifu ya Chuo cha St Joseph, ambapo wanafunzi walionyesha ubunifu wa teknolojia mbalimbali za uhandisi.

Profesa Mkumbo alisema chuo hicho kwa muda mrefu kimekuwa mstari wa mbele kutoa wataalamu wa sayansi na kukitaka kuendelea kuchukua nafasi yake miongoni mwa vyuo vinavyotoa wataalamu wengi wa fani hiyo nchini. Alisema ametembelea maonesho ya kitaaluma ya wanafunzi na kubaini kuwa wamebuni vitu mbalimbali ambavyo vinaweza kuwa na manufaa kwa taifa.

“Nimejionea ubunifu mkubwa sana kwa wanafunzi wenu, lakini kinachosikitisha ni kuwa ubunifu huo unaishia kuwa wazo tu, haufikii mwisho. Nawapa changamoto mhakikishe ubunifu wa wanafunzi wenu unaunganishwa na viwanda na kuwa halisi,” alisema.

“Haitakuwa na maana kama mtakuwa mnabuni vitu lakini vinaishia kwenye vyuo vyenu. Lazima kuwe na utaratibu wa kuhakikisha mnatumia bunifu hizo kuzalisha, wanafunzi wakimaliza hapa wanakwenda kujiajiri au kuajiriwa,” alisema.

Alisema wanafunzi wa vyuo vya sayansi wanapaswa kuendelea kubuni vitu nafuu vitakavyosaidia kutatua changamoto mbalimbali za jamii, akieleza kufurahishwa na ubunifu wa wanafunzi hao wa kutumia nishati safi ya kupikia majumbani wakati ambapo nishati hiyo imekuwa ajenda ya Serikali.

“Rais Samia Suluhu Hassan amekuwa akifanya jitihada kubwa kuhakikisha wananchi wake wanatumia nishati safi ya kupikia. Kwa hiyo nilipoona nanyi mmebuni matumizi ya nishati safi nilifurahi sana, nawapongeza sana,” alisema.

Aidha, alimpongeza Makamu Mkuu wa chuo hicho na menejimenti kwa kuanzisha vituo vitano vya uhamiri vinavyofundisha masuala ya sayansi katika maeneo mbalimbali nchini. “Mnapojikita kwenye matumizi ya roboti na akili mnemba mnakwenda sambamba na dunia inakoelekea kwa sasa. Serikali inakwenda kutekeleza Dira 2050 na moja ya mambo yanayozingatiwa ni matumizi ya teknolojia,” alisema.

Alimpongeza mwanzilishi wa chuo hicho kwa uamuzi wa kuanzisha chuo nchini wakati sekta binafsi haikuwa imekubalika kwa kiwango kikubwa kama ilivyo sasa. Alisema St Joseph ni miongoni mwa vyuo vinavyoongoza katika kufundisha masomo ya sayansi na kuwataka viongozi wake kuhakikisha kinaendelea kuwa kinara katika eneo hilo.

“Kwenye vyuo vinavyofundisha masomo ya sayansi St Joseph mnaongoza, kwani ndio mlianza kufundisha masomo haya kabla ya wengine. Naomba mhakikishe mnabaki kwenye nafasi yenu ya kuwa kinara wa kufundisha masomo ya sayansi,” alisema.





Top News