Na Victor Masangu, Kibaha

Mwenyekiti wa Jumuiya ya wawake (UWT) Wilaya ya Kibahaa mjini Elina Mgonja Katika kuuunga juhudi za Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuwakomboa wanawake kiuchumi ameamua kutoa mafunzo ya ujasiriamali kwa vitendo kwa wanawake wapatao 400 wa Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha Mkoa wa Pwani kwa lengo la kuondokana na wimbi la umasikini.

Akizungumza katika ziara yake maaalumu ya kikazi yenye lengo la kuwatembelea wanawake wa (UWT) katika kata mbali mbali kwa ajili ya kuwapa maarifa na ujuzi na kujifunza jinsi ya kutengeneza bidhaa za aina tofauti ambazo zitawapa fursa ya kujiajiri wao wenyewe na kuondokana na kuwa tegemezi kila kukicha.

Elina amebainisha kuwa amefanya ziara hiyo ikiwa ni utekelezaji wa ahadi yake ambayo aliitoa ya kuwasaidia wanawake wa UWT kutoka kata zote 14 zilizopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha na kwamba mafunzo hayo ambayo ameamua kuyatoa bure bila malipo yoyote yatakuwa ni mkombozi mkubwa katika kujikwamua kiuchumi,

Nao baadhi ya wanawake ambao wamepata mafunzo hayo akiwemo Mwajuma Makuka wamesema kwamba maffunnzo hayo yataweza kuwasaidia kwa kiasi kikubwa kuondokana na kuwa tegemezi na kwamba watakwenda kuyafanyia kazi kwa hali na mali kwa lengo la kuweza kuondokana na wimbi la umasikini.

"Kwa kweli tunapenda kumshukuru kwa dhati Mwenyekiti wetu wa UWT Wilaya ya Kibaha mjini Elina Mgonjwa kwa kuweza kufanya ziara hii na kuja kutupa elimu na mafunzo ya ujasiliamali na tumeweza kujifunza mambo mbali mbali ikiwemo kutengeneza bidhaa kama vile kutengeneza batiki, sabuni za kufulia, sabuni za kuogea pamoja na kupata ujuzi ambao tutakwenda kuufanyia kazi katika kutekeleza majukumu yetu,"amebainisha Mwajuma.

Mwenyekiti huyo wa UWT anaendelea na ziara yake ya kikazi ambapo hadi sasa ameshatembelea kata 7 ambazo ni Msangani, Mkuza, Tumbi, Maili moja, Kongowe, Kibaha pamoja na Kata ya Misususugu ambapo jumla ya wanawake 400 wameweza kunufaika na mafunzo hayo ya ujasiriamali kwa vitendo.









Na. Jordan Mbwambo, WF, Dodoma.

Wizara ya Fedha kwa kushirikiana na Taasisi ya Saratani Ocean Road imeanza kutekeleza zoezi la utoaji wa elimu kuhusu saratani pamoja na vipimo vya uchunguzi wa awali wa saratani kwa watumishi wa Wizara hiyo ili kuongeza uelewa wa namna ya kujikinga, kutambua dalili za awali na kuchukua hatua stahiki kukabiliana na ugonjwa huo.

Zoezi hilo litakalohusisha utoaji wa elimu kuhusu saratani mbalimbali, ikiwemo saratani ya matiti, tezi dume na shingo ya kizazi, pamoja na vipimo vya awali linatarajiwa kufanyika kuanzia tarehe 10 hadi 14 Agosti 2026, katika Ofisi za Wizara ya Fedha, Mtumba, jijini Dodoma.

Akizungumza wakati akifungua mafunzo hayo, Mkurugenzi wa Usimamizi wa Mali za Serikali, Wizara ya Fedha, Bw. Chotto Sendo, alisema ni muhimu kwa watumishi kufuatilia elimu ya afya ya saratani ili kuwa na uelewa wa kutosha kukabiliana na ugonjwa huo.

‘‘Ni muhimu kuwa na uelewa sahihi kuhusu saratani, hususan kwa kuzingatia kwamba utambuzi wa ugonjwa huo katika hatua za awali una nafasi kubwa katika matibabu na kuokoa maisha’’’ Alisema Bw. Sendo.

Aliwasisitiza watumishi wa Wizara hiyo kutumia fursa hiyo kupata elimu pamoja na kufanya vipimo vya awali vinavyotolewa ili kufahamu hali zao za afya.

Kwa upande wake Daktari Bingwa wa Saratani, Taasisi ya Saratani Ocean Road, Dkt. Frank Ruta, aliwahimiza watumishi hao kutopuuza mabadiliko au dalili zisizo za kawaida katika miili yao na kufika katika vituo vya afya kwa ajili ya uchunguzi na ushauri wa kitaalamu.

Alisema utambuzi wa saratani katika hatua za awali unaongeza nafasi ya mafanikio ya matibabu, hivyo jamii inapaswa kujenga utamaduni wa kufanya uchunguzi wa afya mara kwa mara na kuchukua hatua za mapema katika kuzuia na kukabiliana na saratani.

Dkt. Ruta alisemna elimu hiyo ni sehemu ya jitihada za kuimarisha uelewa wa watumishi na jamii kwa ujumla kuhusu afya na kuwahamasisha kuchukua hatua za mapema katika kuzuia na kukabiliana na saratani.

Mkurugenzi wa Idara ya Usimamizi wa Mali za Serikali, Wizara ya Fedha, Bw. Chotto Sendo, akizungumza katika zoezi la utoaji wa elimu kuhusu saratani pamoja na vipimo vya uchunguzi wa awali wa saratani kwa watumishi wa wizara hiyo, linalofanyika katika Ofisi za Wizara ya Fedha, Mtumba, jijini Dodoma, kuanzia tarehe 10 hadi 14 Agosti 2026.

Afisa Utumishi Mwandamizi, Wizara ya Fedha, Bw. Salum Said, akifafanua jambo katika zoezi la utoaji wa elimu kuhusu saratani pamoja na vipimo vya uchunguzi wa awali wa saratani kwa watumishi wa Wizara hiyo, linalofanyika katika Ofisi za Wizara ya Fedha, Mtumba, jijini Dodoma, kuanzia tarehe 10 hadi 14 Agosti 2026.




Daktari Bingwa wa Saratani kutoka Taasisi ya Saratani Ocean Road, Dkt. Frank Ruta, akitoa elimu kuhusu kinga, utambuzi na matibabu ya saratani kwa watumishi wa Wizara ya Fedha, katika zoezi linalofanyika katika Ofisi za Wizara ya Fedha, Mtumba, jijini Dodoma, kuanzia tarehe 10 hadi 14 Agosti 2026.



Baadhi ya Watumishi wa Wizara ya Fedha wakifuatilia elimu iliyokuwa inatolewa na wataalamu kutoka Taasisi ya Saratani Ocean Road, kuhusu namna ya kujikinga, kutambua dalili za awali na kuchukua hatua stahiki katika kukabiliana na ugonjwa wa saratani, katika zoezi linalofanyika katika Ofisi za Wizara ya Fedha, Mtumba, jijini Dodoma, kuanzia tarehe 10 hadi 14 Agosti 2026.


(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, WF, Dodoma)

 Na. Josephine Majura na Asia Singano, WF – Dodoma.


Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), amesema Serikali itaendelea kuimarisha mifumo ya bajeti na usimamizi wa fedha za umma kwa kuzingatia usawa wa kijinsia, hatua inayolenga kuhakikisha rasilimali za Serikali zinatumika kwa ufanisi katika kuchochea maendeleo jumuishi.

Mhe. Balozi Omar (Mb), aliyasema hayo jijini Dodoma, alipokutana na kufanya mazungumzo na Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Usawa wa Kijinsia na Uwezeshaji wa Wanawake (UN Women), nchini Tanzania, Bi. Julia Broussard, katika Ukumbi wa Mikutano wa Waziri wa Fedha, Treasury Square jijini Dodoma.

Mazungumzo hayo yalilenga kuimarisha ushirikiano wa kimkakati kati ya Wizara ya Fedha na UN Women, hususani katika utekelezaji wa Bajeti inayozingatia Masuala ya Kijinsia (Gender-Responsive Budgeting – GRB).

‘’Serikali ya Tanzania, inatambua umuhimu wa kuzingatia masuala ya kijinsia katika sera za fedha, mchakato wa uandaaji wa bajeti, ugawaji wa rasilimali na ufuatiliaji wa utekelezaji wa programu za Serikali ili kuhakikisha mipango ya kitaifa inachangia katika kujenga uchumi jumuishi na wenye usawa’’ alisema Mhe. Balozi Omar (Mb).

Alisema Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2026/2027, imezingatia usawa wa jinsia huku Serikali ikiona umuhimu wa kuandaa Taarifa Maalum ya Bajeti inayozingatia Masuala ya Kijinsia (Gender Budget Statement) kama sehemu ya mfumo rasmi wa usimamizi wa fedha za umma.

Alibainisha kuwa hatua hiyo inaweka msingi wa kuimarisha Mfumo wa Uandaaji wa Bajeti Unaozingatia Masuala ya Kijinsia (GRB), utakaosaidia kuhakikisha masuala ya kijinsia yanaingizwa kikamilifu katika mipango, uandaaji wa bajeti, ugawaji wa rasilimali na ufuatiliaji wa utekelezaji wa programu za umma.

“Muhimu siyo tu kuangalia kiasi cha fedha kilichotengwa au kutumika, bali pia matokeo yanayopatikana kutokana na rasilimali hizo na kupima matokeo ya matumizi ya fedha za umma’’. Alisema Mhe. Balozi Omar (Mb).

Aliongeza kuwa, katika kuhakikisha rasilimali zinazotengwa kwa ajili ya usawa wa kijinsia na uwezeshaji wa wanawake zinafuatiliwa kwa ufanisi, mfumo wa Gender Budget Tagging unaopangwa kuanzishwa utakuwa nyenzo muhimu ya kubaini, kufuatilia na kuchambua matumizi ya bajeti yanayolenga masuala hayo.

Kwa upande wake, Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Usawa wa Kijinsia na Uwezeshaji wa Wanawake (UN Women), nchini Tanzania, Bi. Julia Broussard alisema Wizara ya Fedha ina nafasi muhimu katika kuhakikisha Tanzania inapata na kutoa taarifa zinazohitajika kuhusu Kiashiria cha 5.c.1 cha Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDG 5), kinachopima uwepo wa mifumo ya kufuatilia na kuweka wazi mgao na matumizi ya rasilimali za umma kwa ajili ya kukuza usawa wa kijinsia na uwezeshaji wa wanawake.

Alisema Shirika hilo litaendelea kushirikiana na Wizara ya Fedha, katika kuimarisha mifumo na uwezo wa kitaasisi unaohitajika ili kuhakikisha masuala ya kijinsia yanaingizwa kikamilifu katika mipango, bajeti na usimamizi wa rasilimali za umma.

Ushirikiano huo unalenga kuimarisha matumizi ya takwimu na taarifa za bajeti katika kufanya maamuzi, kufuatilia rasilimali zinazotengwa kwa masuala ya kijinsia na hatimaye kuhakikisha matumizi ya fedha za umma yanaongeza matokeo chanya kwa wananchi, hususan katika kukuza usawa wa kijinsia na uwezeshaji wa wanawake.

Kikao hicho pia kilihudhuriwa na viongozi Mbalimbali wa Wizara ya Fedha, akiwemo Kamishna Msaidizi, Idara ya Fedha za Nje, Bw. Melckzedek Mbise, Kamishna Msaidizi Idara ya Usimamizi wa Bajeti ya Serikali, Bw. Andambike Mololo pamoja na Wataalamu wengine wa Wizara ya Fedha.
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akiagana na Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Usawa wa Kijinsia na Uwezeshaji wa Wanawake (UN Women), nchini Tanzania, Bi. Julia Broussard, baada ya kumalizika kikao cha Waziri wa Fedha na Ujumbe kutoka Shirika hilo, kilichofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Waziri, Treasury Square jijini Dodoma.
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akiongoza Kikao chake na Ujumbe kutoka Shirika la Umoja wa Mataifa la Usawa wa Kijinsia na Uwezeshaji wa Wanawake (UN Women), Ukiongozwa na Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Usawa wa Kijinsia na Uwezeshaji wa Wanawake (UN Women), nchini Tanzania, Bi. Julia Broussard, ulipomtembelea Ofisini kwake, Treasury Square jijini Dodoma.
Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Usawa wa Kijinsia na Uwezeshaji wa Wanawake (UN Women), nchini Tanzania, Bi. Julia Broussard, akizungumza wakati wa kikao na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), hayupo pichani, alipomtembelea Ofisini kwake, Treasury Square jijini Dodoma.
Kikao cha Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), na Ujumbe wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Usawa wa Kijinsia na Uwezeshaji wa Wanawake (UN Women), nchini Tanzania katika Ukumbi wa Mikutano wa Waziri wa Fedha, Treasury Square jijini Dodoma.
Kamishna Msaidizi, Idara ya Fedha za Nje, Bw. Melckzedek Mbise, (wakwanza kushoto), Kamishna Msaidizi Idara ya Usimamizi wa Bajeti ya Serikali, Bw. Andambike Mololo, (wapili kushoto) pamoja na Wataalamu wengine wa Wizara ya Fedha, wakifuatilia kikao cha Mhe. Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), hayupo pichani, na Ujumbe wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Usawa wa Kijinsia na Uwezeshaji wa Wanawake (UN Women), nchini Tanzania, kilichofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Waziri, Treasury Square jijini Dpodoma.
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), (watano kulia), akiwa katika picha ya pamoja na Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Usawa wa Kijinsia na Uwezeshaji wa Wanawake (UN Women), nchini Tanzania, Bi. Julia Broussard, (watano kushoto), Kamishna Msaidizi, Idara ya Fedha za Nje, Bw. Melckzedek Mbise, (watatu kulia), Kamishna Msaidizi Idara ya Usimamizi wa Bajeti ya Serikali, Bw. Andambike Mololo (wa kwanza kulia), Wataalamu kutoka Wizara ya Fedha, pamoja na wajumbe kutoka UN Women, baada ya kumalizika kikao cha Mhe. Balozi Omar (Mb) na Ujumbe huo.

(Picha na Kitengo Cha Mawasiliano Serikalini, WF - Dodoma)

NA DENIS MLOWE, IRINGA

MANISPAA ya Iringa imepokea rasmi magari mawili yenye thamani ya Sh milioni 240.6 kwa ajili ya kurahisisha usimamizi wa utekelezaji wa miradi ya Uboreshaji wa Miundombinu ya Miji (TACTIC) inayotekelezwa katika manispaa hiyo.

Makabidhiano hayo yamefanyika katika hafla fupi iliyohudhuriwa na Mkuu wa Wilaya ya Iringa, Benjamini Sitta, Mkurugenzi wa Manispaa ya Iringa, Zaina Mlawa, wataalamu wa Manispaa, TARURA pamoja na wadau wanaohusika na utekelezaji wa mradi huo katika viwanja vya manispaa.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Sitta amempongeza Mkurugenzi wa Manispaa ya Iringa kwa juhudi za kusimamia utekelezaji wa miradi ya maendeleo, huku akiwataka wataalamu kuhakikisha miradi inayotekelezwa kupitia TACTIC inakamilika kwa wakati na kwa viwango vinavyotakiwa.

Sitta amesema magari hayo yamenunuliwa na mkandarasi kwa ajili ya shughuli za usimamizi wa mradi na yamekabidhiwa kwa Mhandisi Msimamizi ili kurahisisha ufuatiliaji wa kazi katika maeneo mbalimbali ya mradi.

Amesema baada ya kukamilika kwa mradi, magari hayo yatabaki kuwa mali ya Serikali na kutumika katika shughuli nyingine za Serikali, hivyo akasisitiza umuhimu wa kuyatunza na kuyatumia kwa malengo yaliyokusudiwa.

“Magari haya tunawakabidhi yakiwa mazuri na hali nzuri, yakiwa mapya kwa matumizi tunaomba yawe mazuri ili magari haya yaje kuwa na tija zaidi katika kazi zingine za Serikali,” alisema Sitta.

Aidha Sitta amemtaka Mshauri Elekezi wa mradi kusimamia kwa karibu kazi za mkandarasi ili kuhakikisha Serikali inapata thamani ya fedha na miradi inayokidhi viwango vilivyowekwa.

Mradi wa TACTIC katika Manispaa ya Iringa unahusisha ujenzi wa Soko la Kihesa, Ofisi ya Wahandisi pamoja na uboreshaji wa barabara za Mkimbizi-Bima, Mtwivila, Viziwi na Bontank zenye urefu wa jumla ya kilomita 5.26.

Kwa upande wake Mhandisi wa Manispaa ya Iringa, Rajabu Msangi alisema mradi huo ulianza Novemba 20, 2025 na unatarajiwa kukamilika Februari 11, 2027. Hadi sasa utekelezaji wake umefikia asilimia 20.5.

Alisema gharama ya kazi zinazofanywa na mkandarasi ni Sh bilioni 20.258, huku gharama ya Mshauri Elekezi ikiwa dola za Marekani 550,397.50.

Katika utekelezaji wa mradi huo, ujenzi wa barabara unahusisha ujenzi wa makalavati sita, ambapo matatu tayari yamekamilika, ujenzi wa mifereji, uwekaji wa lami, taa na alama za barabarani,ujenzi wa Ofisi ya Wahandisi unaendelea, huku katika Soko la Kihesa kazi ikiwa imefikia hatua ya ujenzi wa kuta.

Msangi alisema mradi huo umekumbana na changamoto kadhaa, ikiwemo mvua za Desemba hadi Machi 2026 zilizoathiri baadhi ya kazi za udongo na tabaka za barabara, pamoja na kuchelewa kupatikana kwa baadhi ya wataalamu na kutokuwapo kwa mitambo ya kutosha.

Hata hivyo, amesema mkandarasi amechukua hatua za kukabiliana na changamoto hizo kwa kupanga upya ratiba ya kazi na kuongeza kasi ya utekelezaji ili kuhakikisha mradi unakamilika ndani ya muda uliopangwa.

Naye Mkurugenzi wa Manispaa ya Iringa, Zaina Mlawa, amesema utekelezaji wa miradi hiyo ni sehemu ya juhudi za kuboresha huduma na miundombinu katika Manispaa ya Iringa, akiwataka wadau wote kushirikiana kuhakikisha malengo ya mradi yanafikiwa.





Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amemtembelea na kumjulia hali, Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, katika makazi yake, Kawe Jijini Dar es Salaam, leo tarehe 10 Agosti 2026.








Dodoma, 8 Agosti 2026 –
RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema Serikali itaendelea kutafuta na kufungua masoko ya ndani na nje ya nchi kwa ajili ya mazao ya kilimo, mifugo na uvuvi, hatua inayolenga kuwawezesha wazalishaji kupata masoko ya uhakika na kuongeza tija katika sekta za uzalishaji.

Rais Samia ameyasema hayo leo, Agosti 8, 2026, wakati akizungumza katika maadhimisho ya Siku ya Wakulima (Nane Nane) Kitaifa yaliyofanyika katika Viwanja vya John Malecela, Nzuguni, Dodoma. Amesema Tanzania imeendelea kufungua milango zaidi kwa biashara na uwekezaji, huku Serikali ikiweka mazingira wezeshi kwa wazalishaji na wawekezaji wa ndani na nje ya nchi.

Katika kuimarisha uzalishaji wa ndani, Kiwanda cha K4 cha Kilombero Sugar kimetajwa kuwa uwekezaji muhimu katika kuongeza uzalishaji wa sukari nchini, kupunguza utegemezi wa bidhaa hiyo kutoka nje ya nchi na kuchangia katika safari ya Tanzania kuelekea kujitosheleza kwa sukari.

Akizungumza na waandishi wa habari katika Maonesho ya Nane Nane, Meneja wa Mawasiliano na Mahusiano na Wadau wa Kilombero Sugar, Bw. Victor Byemelwa, amesema kampuni inajivunia uwekezaji wa K4 ambao umeongeza uwezo wa uzalishaji wa sukari na unatarajiwa kuchochea ukuaji wa kilimo cha miwa pamoja na uchumi wa maeneo yanayozunguka shughuli za kampuni.

Amesema uwekezaji huo hauishii katika uzalishaji wa sukari pekee, bali pia una uwezo wa kuongeza uzalishaji wa umeme kutokana na matumizi ya mabaki ya miwa, hatua inayoweza kuchangia katika kuimarisha upatikanaji wa nishati na kuongeza mchango wa kampuni katika gridi ya Taifa.

"Uwekezaji wa K4 ni hatua kubwa katika kuongeza uzalishaji wa sukari nchini. Pamoja na kuongeza uzalishaji, unafungua fursa nyingi zaidi kwa wakulima wa miwa, ajira, biashara na shughuli nyingine ndani ya mnyororo wa thamani wa kilimo," amesema Byemelwa.

Ametoa wito kwa wananchi, hususan wakulima, kutumia fursa zinazotokana na uwekezaji huo kwa kushiriki kikamilifu katika kilimo cha miwa na shughuli mbalimbali zinazohusiana na mnyororo wa thamani, akisema ukuaji wa sekta ya sukari una uwezo wa kuongeza kipato cha kaya na kuchochea maendeleo ya kiuchumi katika jamii.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Masuala ya Ushirikiano na Mawasiliano wa Kilombero Sugar, Bw. Derick Stanley, amesema kampuni imejipanga kuongeza uzalishaji wa sukari nchini ili kukidhi mahitaji ya soko la ndani na kuchangia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Stanley amesema katika kuongeza uzalishaji wa miwa, Kilombero Sugar inatarajia kushirikiana na wakulima wa nje ya mashamba ya kampuni ambao wanakadiriwa kuzalisha takribani tani milioni 1.5 za miwa, hatua inayotarajiwa kuwawezesha wakulima hao kupata zaidi ya shilingi bilioni 150, hivyo kuongeza kipato cha kaya na kuchochea shughuli za kiuchumi katika maeneo ya uzalishaji.

"Tunaendelea kuangalia fursa za kuongeza uzalishaji na kujenga uwezo wa muda mrefu wa sekta ya sukari. Uwekezaji huu unalenga si tu kuongeza uzalishaji wa sukari, bali pia kuimarisha mnyororo wa thamani, kuongeza fursa kwa wakulima na kuchangia katika maendeleo ya viwanda nchini," amesema Stanley.

Akizungumzia ushiriki wa Kilombero Sugar katika Maonesho ya Nane Nane jijini Dodoma, Mkurugenzi wa Biashara wa Kilombero Sugar, Bw. Fimbo Butala, amesema pia kampuni imetumia maonesho hayo kusogeza bidhaa na huduma zake karibu na wananchi, huku ikitoa elimu kuhusu uzalishaji wa sukari, kilimo cha miwa na mchango wa kampuni katika maendeleo ya sekta ya kilimo na viwanda.

Amesema Nane Nane ni jukwaa muhimu la kukutana moja kwa moja na wakulima, wateja na wadau wengine wa sekta ya kilimo, kusikiliza maoni yao na kujenga ushirikiano unaolenga kukuza uzalishaji na kuongeza thamani katika mnyororo wa kilimo.


Na Mwandishi Wetu
MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kivukoni, Wilaya ya Kinondoni, Dar es Salaam, imemhukumu mfanyabiashara Frank Kagale kifungo cha miaka 20 jela baada ya kumtia hatiani kwa kosa la kukwepa kodi na kuisababishia Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) hasara ya Sh milioni 971.9.

Aidha, mafundi wa mashine za kielektroniki EFD, Awadhi Mhavile (28), Ally Msesya (30), maarufu Ally Yanga, na Msimamizi wa Gereji, Salma Ndauka (26), wameachiwa huru baada ya Jamhuri kushindwa kuthibitisha mashtaka dhidi yao.

Hukumu hiyo ilitolewa mwishoni mwa wiki na Hakimu Mkazi Mfawidhi, Is-haq Kuppa, baada ya kupitia ushahidi, utetezi, vielelezo pamoja na sheria zilinazohusiana na mashtaka hayo.

Hakimu Kuppa alisema Kagale ametiwa hatiani kwa makosa matatu likiwamo la kuisababishia Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) hasara, kukwepa kulipa kodi na kudanganya mfumo wa kielektroniki.

"Kosa la kusababisha hasara, sheria inaelekeza adhabu ya kifungo kisichopungua miaka 20 na kisichozidi miaka 30, huku kosa la kukwepa kulipa kodi likiwa na adhabu ya kulipa mara mbili ya kiasi cha kodi kinachodaiwa au kifungo cha miaka mitatu,"alisema Hakimu Kuppa

Kuhusu kosa la kusababisha hasara, alisema Mahakama imemtia hatiani na inakuhukumu kutumikia kifungo cha miaka 20 na kwa kosa la kukwepa kulipa kodi, adhabu yake ni kulipa mara mbili ya kiasi kinachodaiwa au kutumikia kifungo cha miaka mitatu.

"Kutokana na makosa haya kuhusiana kwa karibu, adhabu hizo zitatumikia kwa pamoja, hivyo Kagale atatumikia kifungo cha miaka 20 jela,"alisema Hakimu Kuppa

Kabla ya kutolewa kwa hukumu hiyo, Wakili wa Serikali, Dickson Swai, aliiomba mahakama kutoa adhabu kali kwa mshtakiwa kutokana na ukubwa wa hasara iliyosababishwa kwa Serikali.

Swai alisema Serikali imepata hasara ya Sh. 971,977,771.32, fedha ambazo zilipaswa kutumika katika shughuli mbalimbali za maendeleo kupitia ukusanyaji wa mapato ya ndani.

“Mheshimiwa, nchi imepata hasara ya Sh .971,977,771.32. Fedha hii imeleta pigo kwa uchumi wa Taifa kwa sababu Serikali inategemea ukusanyaji wa kodi ambao fedha hizo zilipaswa kuingia katika miradi mbalimbali nchini,” alidai Wakili Swai

Pia, alisema kosa hilo lina athari kwa uchumi wa nchi, hasa kutokana na umuhimu wa TRA katika ukusanyaji wa mapato ya ndani.

Swai aliiomba mahakama kutoa adhabu kali ili iwe fundisho kwa Kagale na jamii kwa ujumla, akisisitiza kuwa kutokuwa na historia ya makosa ya jinai hakumaanishi mshtakiwa asipewe adhabu inayostahili kutokana na uzito wa makosa aliyotiwa hatiani.

Kwa upande wa utetezi, waliomba mahakama impunguzie Kagale adhabu kwa kuwa ni mkosaji wa mara ya kwanza, kijana na tegemezi la familia na kwamba mahakama izingatie mazingira yake wakati wa kutoa adhabu.

Naye mshtakiwa Kagale alipopewa nafasi na Mahakama, aliiomba mahakama impunguzie adhabu, kwa sababu hajawahi kufanya kosa la jinai, analijutia kosa hilo na pia ana familia inayomtegemea, wakiwamo wazazi wake wazee, mke na watoto wadogo.

Pia aliiomba mahakama izingatie hali yake ya kiafya, akieleza kuwa anasumbuliwa na pumu na kwamba awali aliwasilisha cheti cha matibabu mahakamani na pia

Mahakama izingatie muda aliokaa mahabusu, akisema amekuwa mahabusu kwa takribani miaka mitatu.

Hata hivyo, Hakimu Kuppa alisema mahakama imezingatia uzito wa makosa, mazingira ya tukio pamoja na hoja zilizowasilishwa na pande zote kabla ya kutoa adhabu hiyo, huku akisisitiza umuhimu wa kuheshimu sheria.

Awali, upande wa mashtaka ulidai kuwa kati ya Mei 17 na Julai mwaka juzi, washtakiwa walitumia mashine za kielektroniki za kutolea risiti (EFD) zilizozuiwa, kutoa risiti zisizo halali na kuisababishia TRA hasara.

Katika shtaka jingine, ilidaiwa kuwa kati ya Mei na Julai mwaka jana, washitakiwa walitumia mashine hizo kumdanganya Kamishna wa Kodi na kuwawezesha baadhi ya walipakodi kunufaika kwa njia isiyo halali, jambo lililosababisha TRA kupata hasara ya Sh 971,977,771.

Shauri hilo liliendeshwa na mawakili wa Serikali John Mwakifuna na Dickson Swai, huku TRA ikiwasilishwa na mawakili Auni Chilamula na Medalakini Emmanuel.

Baada ya hukumu, Wakili Chilamula aliwataka wananchi kuzingatia sheria za kodi, akiwataka wafanyabiashara kutoa risiti halali na wananchi kuchukua risiti halali wanapofanya manunuzi.

Alisema hatua hiyo ni muhimu katika kuhakikisha mapato ya ndani yanaendelea kukusanywa kwa ajili ya kuendesha shughuli za Serikali na kujenga Taifa linalojitegemea
Na Mwandishi Wetu
WANAFUNZI 85 wanatarajia kwenda kusoma katika vyuo mbalimbali nchini India kuanzia wiki ijayo kupitia Wakala wa Elimu Nje ya Nchi Global Education Link (GEL).

Wanafunzi hao na wazazi wao walihudhuria mkutano katika ofisi za GEL mwishoni mwa wiki, ambapo walipewa mafunzo kuhusu namna ya kuishi nchini humo, mambo ya kufanya na kutofanya, pamoja na masuala ya vibali, bima na makaazi.

Mbali na mafunzo hayo, wanafunzi hao walipewa tiketi za ndege, visa na nyaraka mbalimbali zitakazowawezesha kupokelewa katika vyuo wanavyokwenda kusoma. Wanatarajiwa kuanza kwenda India Agosti 21 na 23 mwaka huu.

Akizungumza kwenye mkutano huo, Mkurugenzi Mkuu wa GEL, Abdulmalik Mollel, aliwataka wanafunzi hao kulenga kupata GPA nzuri, lakini pia kutumia muda wao kutafuta fursa zitakazowasaidia baada ya kuhitimu.

“Tunahitaji GPA nzuri lakini pia huko kuna fursa nyingi sana. Mtasoma na watoto wa matajiri wenye viwanda, tunataka muwe karibu na watu kama hao kutambua fursa ya wewe kupata kazi, siyo unamaliza halafu unakuja kuhangaika kutafuta kazi wakati huko kulikuwa na fursa,” alisema.

Mollel aliwataka pia kuchagua marafiki wanaoongeza thamani katika masomo yao na kutumia fursa ya kukutana na wanafunzi kutoka mataifa mbalimbali kujifunza fursa zilizopo katika nchi zao.

Alisema India ina viwanda vidogo vidogo vinavyoweza kuanzishwa kwa mitaji midogo na kuwataka wanafunzi kuondokana na dhana kwamba kuanzisha biashara kunahitaji mabilioni ya fedha.

“India wameendelea sana kwa viwanda. Tumieni fursa hiyo ila isikutoe kwenye reli ya masomo yako. Jiulize unasoma kwa ajili ya GPA nzuri tu au unakwenda kuhamisha maarifa, kuchukua teknolojia na fursa za viwanda zinazopatikana kule kuleta hapa Tanzania,” alisema.

Alisema kila mwaka zaidi ya wanafunzi 800 hupitia GEL kwenda kusoma nje ya nchi na kwamba kuanzia mwakani taasisi hiyo itafungua fursa za ajira kwa kushirikiana na kampuni kubwa nchini zinazohitaji wataalamu mbalimbali.

Mollel alisema wanafunzi wanapaswa kuangalia pia fursa za ajira katika mataifa mengine, akitoa mfano wa Ulaya ambako kuna uhitaji wa rasilimali watu kutokana na watu wengi kustaafu.

“Ulaya kuna shida kubwa ya rasilimali watu kutokana na wengi kustaafu kwa umri. Sasa wewe ukisoma uhandisi jiongeze, soma na Kijerumani au Kifaransa, angalia lugha ambayo inaweza kukusaidia kupata ajira,” alisema.

Alisisitiza kuwa wanafunzi hao wasisome kwa ajili ya GPA pekee, bali warejee Tanzania wakiwa na maarifa, teknolojia na fursa zitakazowasaidia kujiajiri na kupunguza tatizo la ajira.



Na Mwandishi Wetu

MAMLAKA ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imekanusha taarifa zinazosambaa katika mitandao ya kijamii kuhusu hali ya baridi nchini, zikidai kuwa kuanzia kesho saa 11:00 alfajiri kwa muda wa saa 27 kutashuhudiwa tukio la Aphelion litakaloambatana na baridi kali kuliko kawaida.

TMA imesema taarifa hiyo ni potofu, huku ikifafanua kuwa tukio la Aphelion ni hali ya kawaida katika mzunguko wa Dunia kwenye mfumo wa Jua (Solar System), inayotokea kila mwaka na kuhusisha Dunia kuwa mbali zaidi na Jua.

Kwa mujibu wa TMA, mchango wa tukio hilo katika mwenendo wa hali ya baridi kati ya msimu mmoja na mwingine ni mdogo sana katika maeneo ya Tanzania kutokana na nchi hiyo kuwa karibu na Ikweta.

TMA imesema kwa kawaida, kipindi cha miezi ya Juni hadi Agosti kila mwaka ni majira ya Kipupwe katika maeneo mengi nchini, ambapo mifumo ya hali ya hewa hutawaliwa na hali ya baridi na upepo mkali.

Aidha, imesema utabiri wa msimu wa Kipupwe uliotolewa Mei 25, 2026 unaonesha kuwa hali ya baridi ya wastani hadi joto kiasi inatarajiwa katika maeneo ya Kanda ya Ziwa Victoria, Kanda ya Magharibi, Kanda ya Kusini, Nyanda za Juu Kusini Magharibi pamoja na Mkoa wa Singida.

Kwa mujibu wa utabiri huo, hali ya joto kiasi hadi baridi ya wastani inatarajiwa katika maeneo ya Ukanda wa Pwani ya Kaskazini na maeneo ya nchi kavu, Nyanda za Juu Kaskazini Mashariki, Ukanda wa Pwani ya Kusini pamoja na Mkoa wa Dodoma.

TMA imesema vipindi vya baridi zaidi vilitarajiwa kujitokeza mwezi Julai 2026.

Viwango vya joto la chini vinatarajiwa kuwa kati ya nyuzi joto 6°C hadi 21°C katika maeneo ya Nyanda za Juu Kusini Magharibi, kati ya nyuzi joto 10°C hadi 20°C katika maeneo ya Nyanda za Juu Kaskazini Mashariki, kati ya nyuzi joto 8°C hadi 22°C katika maeneo ya Kanda ya Kusini na kati ya nyuzi joto 10°C hadi 25°C katika maeneo mengine ya nchi yaliyosalia.

TMA imewakumbusha wananchi kuwa kwa mujibu wa Sheria ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania Na. 2 ya Mwaka 2019, TMA ndiyo taasisi pekee yenye jukumu na mamlaka ya kutoa taarifa za utabiri na tahadhari za hali ya hewa kwa umma.

Imeeleza kuwa ni kosa kisheria kutoa au kusambaza taarifa zisizo rasmi kwa mujibu wa vifungu vya 27, 31(5) na 46(1) vya Sheria hiyo.

TMA imetoa ufafanuzi huo Dar es Salaam, Agosti 9, 2026, kufuatia taarifa iliyosambaa katika mitandao ya kijamii ikidai kuwa tukio la Aphelion lingesababisha baridi kali kuliko kawaida, hali ambayo ingeweza kusababisha mafua, kikohozi na matatizo ya kupumua.

📍Taasisi 300 kukaguliwa uzingatiaji wa sheria za utumishi wa umma

Serikali imeanza rasmi Ukaguzi wa Uzingatiaji wa Sheria katika Usimamizi wa Utumishi wa Umma kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027, unaolenga kuhakikisha Taasisi za Serikali zinafuata sheria, kanuni, taratibu na miongozo katika usimamizi wa masuala ya kiutumishi na kiutawala.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais - Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete amebainisha  hayo leo Agosti 10, 2026 Jijini Dar es Salaam, wakati akitoa taarifa kuhusu kuanza kwa ukaguzi huo unaotekelezwa na Tume ya Utumishi wa Umma.

Amesema ukaguzi huo ni utekelezaji wa jukumu la Tume kwa mujibu wa Kifungu cha 12(1)(c) cha Sheria ya Utumishi wa Umma, Sura ya 298, kinachoipa Tume mamlaka ya kufanya ukaguzi kwa lengo la kufuatilia na kutathmini kiwango cha uzingatiaji wa sheria, kanuni, taratibu na miongozo ya usimamizi wa masuala ya kiutumishi na kiutawala katika Utumishi wa Umma.

Ameeleza ukaguzi huo unaanza leo, Agosti 10, 2026, na utafanyika katika Taasisi 300 za Serikali, zikiwemo Mamlaka za Serikali za Mitaa 105, Taasisi za Serikali Kuu 78 na Taasisi za Umma 117, zilizopo katika Mikoa 16 nchini.

Mikoa itakayohusishwa katika ukaguzi huo ni Mwanza, Dodoma, Dar es Salaam, Arusha, Mara, Iringa, Morogoro, Lindi, Simiyu, Kilimanjaro, Shinyanga, Manyara, Songwe, Tanga, Kagera na Geita.

Aidha, Mhe. Ridhiwani amewataka Waajiri katika Taasisi zote zitakazofanyiwa ukaguzi kushirikiana na Tume ya Utumishi wa Umma kwa kutoa ushirikiano na taarifa zinazohitajika ili kuwezesha ukaguzi huo kufanyika kwa ufanisi.

Amesisitiza kuwa ukaguzi huo ni sehemu ya jitihada za Serikali za kuimarisha uwajibikaji, utawala bora na uzingatiaji wa sheria katika Utumishi wa Umma, hatua ambayo itasaidia kuboresha usimamizi wa rasilimali watu na utoaji wa huduma kwa wananchi.














 


Top News