SERIKALI imesema kima cha chini cha mshahara katika sekta binafsi nchini huwekwa kwa kuzingatia sekta za kiuchumi pamoja na vigezo mbalimbali vya kisheria, huku ikisisitiza kuwa utaratibu huo haujajengwa kwa lengo la kubagua wafanyakazi wa kampuni za kigeni na zile za kizawa.
Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano) Deus Sangu wakati akijibu swali la Mbunge wa Kuteuliwa, Mheshimiwa Abdulliah Ali Mwinyi, aliyehoji iwapo Serikali haioni kuwa utofauti wa viwango vya kima cha chini cha mshahara kati ya kampuni za kigeni na za kizawa unaweza kutengeneza tabaka katika jamii.
Katika swali lake, Mbunge huyo alitaka kujua kama Serikali haioni kuwa kanuni zinazoweka viwango tofauti vya mishahara kwa kampuni za kigeni na za kizawa zinaweza kuleta ubaguzi katika ajira na malipo ya wafanyakazi.
Akijibu, Waziri amesema kima cha chini cha mshahara kinawekwa kwa mujibu wa Sheria ya Taasisi za Kazi, Sura ya 300, ambayo imeanzisha Bodi za Kima cha Chini cha Mshahara kwa kuzingatia sekta mbalimbali za uchumi.
Waziri Sangu amesema katika Sekta Binafsi, Bodi ya Kima cha Chini cha Mshahara ina jukumu la kufanya tafiti kuhusu hali ya ajira na uchumi na kumshauri Waziri mwenye dhamana ya masuala ya kazi kuhusu kiwango kinachopaswa kuwekwa na kutangazwa kwa sekta husika.
Waziri amesema kima cha chini cha mshahara katika sekta binafsi nchini hakipangwi kwa mtazamo wa kampuni kuwa ya kigeni au ya kizawa pekee, bali huzingatia sekta za kiuchumi ambazo waajiri na wafanyakazi wanafanyia kazi.
Aidha, amesema katika kupanga viwango hivyo, Serikali huzingatia vigezo mbalimbali vilivyowekwa na mikataba ya kimataifa pamoja na sheria za nchi, ikiwemo uwezo wa waajiri kufanya biashara na kulipa ujira unaostahili.
Kigezo kingine kinachozingatiwa, kwa mujibu wa Serikali, ni gharama za maisha, jambo linalolenga kuhakikisha viwango vya mishahara vinazingatia mazingira halisi ya kiuchumi yanayowakabili wafanyakazi na waajiri.
Kauli hiyo ya Serikali imekuja wakati ambapo suala la tofauti za mishahara katika sekta binafsi likiwa miongoni mwa hoja zinazogusa usawa katika ajira, uwezo wa waajiri na ustawi wa wafanyakazi.
Serikali imeendelea kusisitiza kuwa upangaji wa kima cha chini cha mshahara unapaswa kuzingatia hali ya uchumi, gharama za maisha na uwezo wa waajiri, huku ukiendana na matakwa ya sheria za nchi na mikataba ya kimataifa ya kazi.




.jpeg)

.jpeg)










.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)




.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)
