Wananchi wa Kata ya Mpandangindo katika Jimbo la Peramiho wanatarajia kunufaika na ujenzi wa barabara ya Mpandangindo kupitia Parangu hadi Peramiho, baada ya Serikali kutenga zaidi ya shilingi milioni 250 kwa ajili ya utekelezaji wa mradi huo.

Akizungumza na wananchi, Mbunge wa Jimbo la Peramiho, Mhe. Dkt. Lazaro Komba Bunungu, amewahakikishia kuwa ujenzi wa barabara hiyo utaanza, akieleza kuwa mradi huo ni sehemu ya jitihada za Serikali kuboresha miundombinu na kurahisisha shughuli za kijamii na kiuchumi.

Mhe. Dkt. Bunungu amesema barabara hiyo imekuwa kero kwa muda mrefu kutokana na hali yake kutokuwa nzuri, jambo ambalo limekuwa likikwamisha usafiri na usafirishaji wa mazao pamoja na shughuli nyingine za maendeleo kwa wananchi.

Kwa upande wake, Mhandisi wa TARURA, Simon Binamu, amesema tayari bajeti ya zaidi ya shilingi milioni 250 imetengwa kwa ajili ya ujenzi wa barabara hiyo, na kwamba kwa sasa mradi upo katika hatua za utekelezaji.

Ujenzi wa barabara hiyo unatarajiwa kuboresha mawasiliano kati ya Mpandangindo, Parangu na Peramiho, kurahisisha usafiri wa wananchi, kuongeza fursa za biashara na kuchochea maendeleo ya kiuchumi katika maeneo hayo.




Na Peter Ngamilo- TAEC

Katika safari ya Tanzania kuelekea uchumi wa kisasa na wa viwanda, sekta za kilimo, mifugo na viwanda zinaendelea kuwa nguzo muhimu za maendeleo ya Taifa. Hata hivyo, ukuaji wa sekta hizo hauwezi tena kutegemea mbinu za jadi pekee, hasa katika kipindi ambacho dunia inakabiliwa na changamoto za ongezeko la watu, mabadiliko ya tabianchi, kupungua kwa rutuba ya ardhi, uhaba wa maji pamoja na kuongezeka kwa magonjwa ya mimea na mifugo.

Mataifa mbalimbali duniani yameamua kukabiliana na changamoto hizo kwa kuwekeza katika sayansi na teknolojia. Miongoni mwa teknolojia zinazobadili taswira ya uzalishaji wa chakula na usimamizi wa rasilimali ni teknolojia ya nyuklia, ambayo kwa miongo kadhaa imekuwa ikitumika kuongeza tija katika kilimo, kuboresha uzalishaji wa mifugo, kusimamia rasilimali za maji, kuimarisha tafiti za kisayansi na kuongeza ushindani wa bidhaa katika masoko ya ndani na kimataifa.

Kwa mujibu wa Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano wa Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania (TAEC), Peter Ngamilo, bado kuna uelewa mdogo miongoni mwa wananchi kuhusu mchango wa teknolojia ya nyuklia katika maendeleo ya kila siku.

“Watu wengi wakisikia neno nyuklia hufikiria uzalishaji wa umeme au silaha. Ukweli ni kwamba sehemu kubwa ya teknolojia hii duniani inatumika kuboresha maisha ya wananchi kupitia kilimo, mifugo, maji, afya na viwanda. Hii ndiyo elimu ambayo TAEC inaendelea kuifikisha kwa wananchi kupitia Maonesho ya Nanenane,” anasema Ngamilo.


Anasema ushiriki wa TAEC katika Maonesho ya Nanenane haulengi tu kuonesha shughuli za Tume, bali pia kuwajengea wananchi uelewa kwamba teknolojia ya nyuklia ni nyenzo ya maendeleo inayoweza kuongeza uzalishaji wa chakula, kupunguza gharama za uzalishaji, kuongeza thamani ya mazao na kuchochea ukuaji wa uchumi.

KILIMO KISICHOTEGEMEA BAHATI, BALI SAYANSI

Sekta ya kilimo ni miongoni mwa nguzo kuu za uchumi wa Tanzania. Hata hivyo, uzalishaji wake bado unakabiliwa na changamoto mbalimbali, zikiwemo wadudu waharibifu, magonjwa ya mimea, matumizi yasiyo sahihi ya mbolea na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Katika nchi mbalimbali duniani, baadhi ya changamoto hizo zimepatiwa suluhisho kupitia matumizi ya teknolojia ya nyuklia, ikiwemo mbinu ya mutation breeding, inayotumika katika kuboresha mbegu ili kupata aina za mazao zenye uwezo wa kustahimili ukame, magonjwa na wadudu, huku zikitoa mavuno bora.

Kwa mujibu wa taarifa za mashirika ya kimataifa yanayohusika na matumizi ya teknolojia ya nyuklia katika kilimo, zaidi ya aina 3,400 za mazao yaliyoboreshwa kwa kutumia mbinu za mutation breeding zimesajiliwa katika zaidi ya nchi 75 duniani.

Nchi kama China, India na Vietnam ni miongoni mwa zilizopata mafanikio katika matumizi ya mbinu hizo, ambapo aina mbalimbali za mazao zimeboreshwa kwa lengo la kuongeza uzalishaji na kukabiliana na changamoto za mazingira.

Ngamilo anasema Tanzania ina sababu ya kuwekeza zaidi katika matumizi ya teknolojia hiyo.

“Tanzania imejaliwa kuwa na ardhi kubwa, rasilimali za maji na mazingira yanayofaa kwa uzalishaji wa mazao mbalimbali. Tukichanganya rasilimali hizi na teknolojia ya kisasa, ikiwemo teknolojia ya nyuklia, tunaweza kuongeza uzalishaji wa mazao ya kimkakati, kupunguza gharama za uzalishaji na kuongeza ushindani wa bidhaa zetu katika masoko ya kikanda na kimataifa,” anasema.

KUPAMBANA NA WADUDU BILA KUHARIBU MAZINGIRA

Kila mwaka wakulima hupoteza sehemu ya mazao kutokana na wadudu waharibifu, hali inayosababisha hasara na kupunguza tija ya kilimo.

Moja ya matumizi muhimu ya teknolojia ya nyuklia katika kudhibiti wadudu ni Sterile Insect Technique (SIT), mbinu inayohusisha uzalishaji na kuachiliwa kwa wadudu wa kiume waliotiwa utasa ili wanapopandana na majike wasiweze kuzalisha kizazi kipya.

Mbinu hiyo imekuwa ikitumika katika maeneo mbalimbali duniani kudhibiti wadudu waharibifu, wakiwemo baadhi ya aina za nzi wanaoshambulia matunda na mazao mengine.

Kwa Tanzania, matumizi ya teknolojia hiyo yanaweza kuwa na mchango katika kudhibiti wadudu waharibifu, kuongeza uzalishaji wa matunda na mboga, kupunguza utegemezi wa viuatilifu na kusaidia kulinda mazingira.

“Teknolojia ya nyuklia inatufundisha kuwa si kila tatizo la kilimo linahitaji matumizi makubwa ya kemikali. Sayansi imetupa mbinu mbadala zinazoweza kusaidia kulinda mazingira na wakati huo huo kuongeza uzalishaji wa mazao,” anasema Ngamilo.

MIFUGO: KUBORESHA AFYA NA KUONGEZA UZALISHAJI

Sekta ya mifugo ina mchango mkubwa katika uchumi wa Tanzania, lakini bado inakabiliwa na changamoto za magonjwa, uzalishaji, uzazi na lishe.

Teknolojia ya nyuklia inaweza kutumika katika uchunguzi na udhibiti wa magonjwa, utafiti wa lishe ya mifugo pamoja na kufuatilia namna virutubisho vinavyotumika mwilini, hatua inayoweza kusaidia kuboresha uzalishaji wa maziwa na nyama.

Mfano unaotajwa katika matumizi ya teknolojia ya nyuklia katika kudhibiti magonjwa ya mifugo ni Zanzibar, ambako matumizi ya Sterile Insect Technique yalichangia katika udhibiti wa nzi tsetse na kupunguza tatizo la trypanosomiasis.

Ngamilo anasema uzoefu huo unaonesha kwamba Afrika inaweza kutumia sayansi na teknolojia kutatua changamoto zinazolikabili bara hilo.

“Mfano wa Zanzibar unaonesha wazi kuwa teknolojia ya nyuklia inaweza kutoa suluhisho la changamoto ambazo kwa miaka mingi zilionekana kuwa ngumu na zenye gharama kubwa kuzitatua. Huu ni ushahidi kwamba teknolojia hii inaweza kuleta matokeo yanayogusa maisha ya wananchi,” anasema.

MAJI: RASILIMALI INAYOHITAJI SAYANSI

Katika kipindi ambacho mabadiliko ya tabianchi yanaendelea kuathiri upatikanaji na usalama wa maji, teknolojia ya nyuklia inaweza kuwa nyenzo muhimu katika usimamizi wa rasilimali hiyo.

Kupitia matumizi ya Isotope Hydrology, wataalamu wanaweza kupata taarifa kuhusu chanzo cha maji, umri wa maji yaliyopo chini ya ardhi, mwelekeo wa mtiririko wake na namna yanavyorejea kwenye mifumo ya asili.

Taarifa hizo zinaweza kusaidia katika kupanga matumizi endelevu ya maji kwa ajili ya kilimo, mifugo, viwanda na matumizi ya binadamu.

“Kilimo cha kesho kitategemea siyo tu upatikanaji wa maji, bali pia uwezo wa kuyatumia kwa ufanisi. Teknolojia ya nyuklia inatupa maarifa ya kisayansi yanayotuwezesha kuelewa na kupanga matumizi bora ya rasilimali hiyo muhimu,” anaeleza Ngamilo.

SAYANSI INAYOENDESHA TAFITI NA VIWANDA

Mbali na kilimo, mifugo na maji, teknolojia ya nyuklia ina nafasi katika tafiti zinazolenga kuboresha rutuba ya udongo, matumizi sahihi ya mbolea na kuongeza ufanisi wa uzalishaji wa mazao.

Katika sekta ya viwanda, teknolojia hiyo inaweza kutumika katika upimaji wa ubora wa bidhaa, ukaguzi wa miundombinu bila kuiharibu pamoja na kuboresha ufanisi wa michakato mbalimbali ya uzalishaji.

Kwa mujibu wa Ngamilo, maendeleo ya viwanda hayawezi kutenganishwa na maendeleo ya kilimo na mifugo kwa sababu viwanda vinahitaji malighafi bora na za kutosha.

“Viwanda vinahitaji malighafi bora. Malighafi bora zinatokana na kilimo na mifugo yenye tija. Hivyo, teknolojia ya nyuklia inaunganisha mnyororo mzima wa thamani, kuanzia shambani hadi kiwandani na hatimaye sokoni,” anasema.

NANENANE: KUWEKEZA KATIKA MAARIFA

Katika Maonesho ya Nanenane mwaka 2026, TAEC inaendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu matumizi salama na yenye manufaa ya teknolojia ya nyuklia katika sekta mbalimbali za maendeleo.

Ngamilo anasema wananchi wanaotembelea banda la TAEC wamekuwa wakionesha hamu ya kufahamu namna teknolojia hiyo inavyoweza kutumika kutatua changamoto zinazowakabili katika shughuli zao za kila siku.

“Tunataka wananchi waondoke katika banda la TAEC wakiwa na uelewa kwamba teknolojia ya nyuklia si teknolojia ya mbali. Ni teknolojia inayoweza kumsaidia mkulima kuongeza mavuno, mfugaji kuongeza uzalishaji wa maziwa na nyama, mtafiti kupata majibu sahihi na Taifa kujenga uchumi imara,” anasema.

TANZANIA INA FURSA YA KUONGOZA

Kwa kuwa na ardhi kubwa, rasilimali za maji, mifugo na nguvu kazi ya vijana, Tanzania ina fursa kubwa ya kutumia sayansi na teknolojia kuongeza uzalishaji wa chakula, kuimarisha usalama wa chakula, kuongeza thamani ya mazao, kukuza mauzo ya nje na kuharakisha ujenzi wa uchumi wa viwanda.

Hata hivyo, fursa hiyo inahitaji uwekezaji zaidi katika tafiti, miundombinu, wataalamu na uhamasishaji wa matumizi ya teknolojia hiyo miongoni mwa wakulima, wafugaji, wafanyabiashara na wadau wengine.

Ngamilo anasisitiza kwamba teknolojia ya nyuklia si mbadala wa mkulima au mfugaji, bali ni nyenzo inayoweza kuongeza tija, ubora na ushindani wa bidhaa zao.

“Safari ya kuelekea Tanzania yenye uchumi wa kisasa haitategemea rasilimali tulizonazo pekee, bali namna tutakavyozitumia kwa kutumia sayansi na teknolojia. Teknolojia ya nyuklia ni moja ya zana muhimu zitakazotuwezesha kufikia azma hiyo. Huu ndio ujumbe tunaoupeleka kwa Watanzania kupitia Maonesho ya Nanenane 2026,” anahitimisha Ngamilo.




Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Obedi Laiser (katikati), pamoja na baadhi ya wachezaji wa timu ya soka ya benki hiyo, wakishangilia mara baada kupokea kikombe kutoka kwa Mweka Hazina wa Chama cha Mabenki Tanzania (TBA) , Bw. Rayson Foya,  baada ya kuibuka na ushindi kwa kuichapa timu ya benki ya Mwanga Hakika kwa bao 1-0 katika mchezo wa fainali za Ligi ya Chama TBA, katika Viwanja vya Gymkhana, jijini Dar es Salaam jana.  
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Obedi Laiser ( wa tatu kushoto), akipokea kikombe kutoka kwa Mweka Hazina wa Chama cha Mabenki Tanzania (TBA) , Bw. Rayson Foya( wa pili kushoto)  baada ya timu ya benki hiyo, kuibuka mshindi kwa kuichapa timu ya benki ya Mwanga Hakika kwa bao 1-0 katika mchezo wa fainali za Ligi ya Chama cha Mabenki Tanzania (TBA Footie Tournament 2026), katika Viwanja wa Gymkhana jijini Dar es Salaam jana.
Ofisa wa Wateja Binafsi wa Benki ya Absa Tanzania , Bw. Paschal John ( kushoto) akipokea tuzo ya mchezaji bora kutoka kwa Mkurugenzi wa Uchunguzi wa Chama cha Mabenki Tanzania (TBA), Bw. Dan Tandasi mara baada ya mchezo wa fainali za Ligi ya Chama cha Mabenki Tanzania (TBA Footie Tournament 2026),  uliyofanyika katika Viwanja wa Gymkhana jijini Dar es Salaam jana.

Picha mbalimbali zikionesha mtifuano mkali dhidi ya wachezaji wa timu za soka za benki ya Absa na Mwanga Hakika, katika mchezo wao wa fainali za Michuano ya TBA Footie Tournament 2026, katika Viwanja vya Gymkhana, jijini Dar es Salaam jana. Absa ilishinda mtanange huo kwa bao 1-0 hivyo kutwaa ushindi wa michuano hiyo kwa mwaka huu. 

Kikosi kabambe cha timu ya soka ya Benki ya Absa, wakipiga picha ya pamoja kabla ya kuanza mchezo wa fainali dhidi ya Mwanga Hakika Bank, katika Viwanja vya Gymkhana, jijini Dar es Salaam jana. Absa ilishinda kwa bao 1-0.

Jeshi la Zimamoto na Uokoaji limeendelea kutoa elimu kwa wananchi wanaotembelea Maonesho ya Kilimo Nanenane Kitaifa jijini Dodoma, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuongeza uelewa kuhusu masuala ya usalama dhidi ya majanga ya moto na namna ya kuchukua tahadhari katika maeneo mbalimbali.

Katika maonesho hayo, wananchi wamepatiwa elimu kuhusu matumizi sahihi ya vifaa vya kuzimia moto pamoja na hatua za kuchukua wakati yanapotokea majanga hususani Jikoni wakati wa kupika kwa kutumia Nishati ya gesi, Jeshi hilo pia limeendelea kutoa elimu ya huduma za uokoaji na umuhimu wa wananchi kutoa taarifa mapema pindi wanapoona majanga mbalimbali ikiwemo moto.

Zoezi hilo ni muhimu katika kuimarisha uelewa wa jamii kuhusu kinga na tahadhari dhidi ya moto, huku wananchi wakihimizwa kuzingatia maelekezo ya wataalamu na kuchukua hatua za usalama katika maeneo ya makazi, biashara na shughuli nyingine za kiuchumi.







Na Janeth Raphael - MichuziTv 

Shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo (FAO) limezindua mfumo wa kidijitali wa TANFISH, unaolenga kuwaunganisha wavuvi, wasindikaji wa samaki na wanunuzi ili kurahisisha biashara ya mazao ya uvuvi na kuwafungulia wazalishaji masoko mapana zaidi ndani na nje ya maeneo yao

Akizungumza katika hafla hiyo iliyofanyika Dodoma, Mtaalamu wa Kimataifa  wa Mnyororo wa thamani wa Uvuvi na Ufugaji wa Viumbe  Maji wa FAO,  Hasheem Muumin, amesema TANFISH inawawezesha wavuvi na wasindikaji kujisajili kwenye mfumo, kuweka picha na taarifa za bidhaa zao na kuwasiliana moja kwa moja na wanunuzi kutoka maeneo mbalimbali nchini.

Amesema mfumo huo unahudumia aina mbalimbali za bidhaa za uvuvi, zikiwemo samaki wabichi, waliokaushwa na waliogandishwa kutoka kwenye maji ya bahari, maziwa pamoja na shughuli za ufugaji wa samaki.

Kwa mujibu wa  Muumin, TANFISH pia imejengwa kwa kuimarisha usalama wa miamala, ikiwemo kulinda malipo ya wanunuzi, huku ikiwawezesha wavuvi na wasindikaji kupata masoko makubwa na yenye uhakika zaidi.

“TANFISH inalinda malipo ya wanunuzi huku ikiwawezesha wavuvi na wasindikaji kupata masoko makubwa na yenye uhakika zaidi,” amesema Dkt. Muumin.

Amesema hadi sasa FAO imewapatia mafunzo zaidi ya wavuvi, wasindikaji na wadau wengine 500, ambao tayari wamesajiliwa katika mfumo huo.

Aidha, zaidi ya tani mbili za samaki tayari zimeuzwa kupitia TANFISH, huku Dodoma ikiwa miongoni mwa masoko makubwa yaliyofikiwa na mfumo huo pamoja na maeneo mengine nchini.

 Muumin amesema TANFISH ilianza kwa kulenga zaidi jamii zinazozunguka Ziwa Tanganyika, lakini sasa imepanuka na kuwajumuisha wasindikaji na wafanyabiashara kutoka Ziwa Victoria pamoja na maeneo ya pwani ya Tanzania, hatua inayolenga kujenga soko la kidijitali la bidhaa za uvuvi linalounganisha maeneo mbalimbali nchini.

Mfumo huo unapatikana kupitia vifaa vya Android na Apple, hivyo kuwawezesha watumiaji kuupata na kufanya biashara kwa urahisi zaidi.

Ili kuhakikisha ubora wa bidhaa na kulinda uaminifu wa watumiaji, wauzaji wanatakiwa kuzingatia matakwa yote ya kisheria na kanuni za Serikali, ikiwemo kuwa na nyaraka halali za biashara.

Kwa upande wa wanunuzi, wanatakiwa kutoa taarifa sahihi za mahali bidhaa zinapopaswa kufikishwa ili kurahisisha usafirishaji na kuhakikisha samaki wanafika kwa usalama na kwa wakati.

Uzinduzi wa TANFISH ni sehemu ya juhudi za FAO za kutumia teknolojia na mifumo ya kidijitali kuimarisha minyororo ya thamani ya kilimo na uvuvi, kuongeza fursa za masoko na kuchochea ongezeko la kipato kwa wazalishaji nchini.







Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) imeanza mazungumzo na wazalishaji wa parachichi katika wilaya za Mufindi na Njombe kwa lengo la kuanzisha mfumo wa ubunifu utakaoruhusu shamba kutumika kama ghala la bidhaa hai ili kuongeza ufanisi wa biashara ya zao hilo.

Mkurugenzi Mtendaji wa WRRB, Bw. Asangye Bangu, amesema hayo katika Maonesho ya Nanenane yanayoendelea kwenye Viwanja vya Dkt. John Malecela jijini Dodoma wakati akitoa maelezo kwa Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Denis Londo, aliyetembelea banda la WRRB.

Bw. Bangu amesema utaratibu huo utahakikisha matunda yanayovunwa ni yale tu yaliyofikia viwango vinavyohitajika na wanunuzi, jambo litakalopunguza upotevu wa mazao baada ya mavuno, kuhifadhi ubora wa bidhaa na kuongeza thamani ya biashara ya parachichi.

Aidha, amesema WRRB inatarajia kushirikiana na Shirika la Posta Tanzania ili kuunganisha Mfumo wa Stakabadhi za Ghala na huduma za kidijitali za biashara pamoja na usafirishaji wa bidhaa.

Amesema ushirikiano huo unatarajiwa kuongeza ufanisi wa biashara, kurahisisha miamala na kuimarisha imani ya wanunuzi katika soko.

Awali, Kaimu Mkurugenzi wa Uratibu Huduma wa WRRB, Bw. Mwita Thomas, amesema mfumo huo unaendelea kupanuliwa kutoka kwenye mazao ya kilimo pekee na sasa unahusisha pia bidhaa zisizo za kilimo, zikiwamo mifugo hai, mwani na samaki wanaofugwa kwenye vizimba.

Serikali mkoani Geita kupitia tume ya umwagiliaji  imesambaza jumla ya pampu 141 za umwagiliaji kwa vikundi 119 vya wakulima wenye takribani wanachama 13,000 katika halmashauri zote za mkoa huo, katika jitihada za kuongeza uzalishaji na kupunguza utegemezi wa mvua.

Akikabidhi pampu hizo kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mkuu wa Wilaya ya Bukombe Paskas Muragili amesema pampu hizo zitaleta kasi kubwa ya uzalishaji kwa wakulima na kuchangia katika mapinduzi ya kilimo mkoani humo.

Ameongeza kuwa ugawaji wa pampu hizo unapaswa kwenda sambamba na ushirikishwaji wa sekta nyingine ikiwemo utoaji wa elimu na mbinu bora za kilimo na pia uhakikishaji wa upatikanaji wa pembejeo kwa wakati.

Kwa upande wake Mhandisi kutoka Timu ya Umwagiliaji mkoa wa Geita, Boniface Mkita amesema pampu hizo zimegharimu jumla ya shilingi bilioni 1.012.

Amefafanua kuwa kupitia mpango huu, eneo lenye ukubwa wa hekari 2,092 litamwagiliwa kwa wakati mmoja. Hii itapunguza utegemezi wa mvua na kupandisha uzalishaji wa zao la mahindi kutoka tni 1 kwa hekari hadi tani 2.5 kwa hekari1 

Mkita amebainisha kuwa mpango huu unatarajiwa kuwanufaisha moja kwa moja wakulima 1,389, kati yao wanawake 369 na wanaume 1,020.

 Serikali imesisitiza kuwa uwekezaji huu ni sehemu ya mkakati wa kuhakikisha Geita inakuwa miongoni mwa mikoa inayolisha Taifa kupitia kilimo cha umwagiliaji.








Na Belinda Joseph, Dodoma

Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Dennis Londo, amesema matumizi ya taarifa sahihi za masoko ni nyenzo muhimu katika kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania, kukuza mauzo ya nje na kuvutia uwekezaji wa kimkakati unaochochea ukuaji wa uchumi.

Mhe. Londo ameyasema hayo Agosti 7, 2026, katika Viwanja vya Nane Nane, jijini Dodoma, wakati akifungua mkutano wa Intelijensia ya Masoko na Matokeo, ulioandaliwa na Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO), uliowakutanisha wadau mbalimbali kujadili namna taarifa za masoko zinavyoweza kutumika kuchochea biashara na maendeleo ya viwanda.

Amesema mabadiliko ya teknolojia, mahitaji ya walaji na mifumo ya uzalishaji na usambazaji yanaendelea kufungua fursa mpya za biashara, hivyo Tanzania inapaswa kuendelea kutumia taarifa za masoko kuwawezesha wazalishaji na wafanyabiashara kufanya maamuzi sahihi na kuongeza ushindani katika masoko ya kikanda na kimataifa.

“Tunapaswa kuzalisha kwa kuzingatia mahitaji ya soko na kutumia taarifa sahihi za masoko katika kufanya maamuzi ya uzalishaji, uwekezaji na biashara,” amesema.

Ameeleza kuwa juhudi za Tanzania kujenga uchumi wa kisasa unaotegemea viwanda na kuongeza mauzo ya bidhaa nje ya nchi zinahitaji ushirikiano madhubuti kati ya Serikali, sekta binafsi na taasisi mbalimbali, ili kuhakikisha wazalishaji na wafanyabiashara wanapata taarifa muhimu za masoko kwa wakati.

Aidha, amesema Serikali itaendelea kuweka mazingira wezeshi kwa biashara na uwekezaji, pamoja na kuhamasisha uzalishaji wa bidhaa zenye ubora na viwango vinavyokidhi mahitaji ya masoko ya kimataifa, hatua itakayosaidia kuongeza thamani ya bidhaa na fursa za mauzo nje ya nchi.

Mhe. Londo amesema matumizi ya taarifa sahihi za masoko yatawawezesha wazalishaji kubaini mahitaji na fursa zilizopo katika masoko mbalimbali, kupanga uzalishaji kulingana na mahitaji ya walaji na kuimarisha uwezo wa bidhaa za Tanzania kushindana katika masoko ya kikanda na kimataifa.

Amesisitiza kuwa mafanikio ya juhudi hizo yanahitaji ushirikiano wa karibu kati ya Serikali na sekta binafsi, huku akieleza kuwa kuunganisha taarifa za masoko na uzalishaji, uongezaji thamani na biashara kutasaidia kuongeza kipato cha wananchi, kutengeneza ajira na kuchochea ukuaji jumuishi wa uchumi.

Akihitimisha hotuba yake, Mhe. Londo amesema matumizi madhubuti ya taarifa za masoko, sambamba na uwekezaji katika uzalishaji na uongezaji thamani, ni msingi muhimu katika kujenga uchumi imara na wenye ushindani, huku Tanzania ikiendelea kutumia fursa zinazotokana na masoko ya kikanda na kimataifa.







Na Belinda Joseph-Dodoma.

Mkurugenzi wa Idara ya Uzalishaji na Maendeleo ya Masoko kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Stephen Michael, amesema Tanzania inalenga kuongeza uzalishaji wa maziwa na kuondokana na utegemezi wa uagizaji wa bidhaa za maziwa kutoka nje kupitia utekelezaji wa Mradi wa Mageuzi ya Tasnia ya Maziwa na Mabadiliko ya Tabianchi (C-SDTP).

Akizungumza na waandishi wa habari Agosti 7, 2026, katika Banda la C-SDTP kwenye Maonesho ya 88 yanayoendelea katika Viwanja vya Dkt. John Malecela jijini Dodoma, Stephen amesema sekta ya maziwa ni miongoni mwa sekta muhimu zinazochangia uchumi wa nchi kupitia sekta ya mifugo.

Amesema tathmini iliyofanyika imebaini kuwa ifikapo mwaka 2030 Tanzania inaweza kukabiliwa na upatikanaji mdogo wa maziwa endapo hakutakuwa na uwekezaji wa kutosha, kutokana na kuongezeka kwa kipato cha wananchi, ongezeko la idadi ya watu na kasi ya ukuaji wa mijini.

Kwa mujibu wa Stephen, Mradi wa C-SDTP wenye thamani ya dola za Marekani milioni 231 utatekelezwa kwa kipindi cha miaka 10, ukiwa na lengo la kuongeza uzalishaji wa maziwa, kuimarisha upatikanaji wa malighafi kwa viwanda vya kusindika maziwa na kuiwezesha Tanzania kubadilika kutoka kuwa muagizaji na kuwa muuzaji wa maziwa katika masoko ya nje.

Amesema mradi huo utatumia mfumo wa corridor approach katika maeneo yenye uwezo mkubwa wa uzalishaji wa maziwa, huku ukizingatia mnyororo wa thamani wa maziwa ili kuongeza uzalishaji, ukusanyaji, usindikaji na upatikanaji wa malighafi kwa viwanda.

Ameainisha kuwa mradi utatekelezwa katika mikoa ya Arusha, Iringa, Mbeya, Njombe, Tanga, Morogoro, Pwani na Kilimanjaro kwa Tanzania Bara, huku Zanzibar ukihusisha mikoa yote mitano ambayo ni Mjini Magharibi, Kaskazini Unguja, Kusini Unguja, Kaskazini Pemba na Kusini Pemba.

Stephen amesema mradi huo pia utatoa kipaumbele kwa vijana, wanawake na watu wenye ulemavu kupitia upatikanaji wa ng’ombe bora wa maziwa kwa ruzuku, ujenzi wa vituo vya ukusanyaji wa maziwa (Milk Collection Centers na Milk Collection Points) pamoja na kuboresha miundombinu ya usafirishaji wa maziwa kutoka kwa wazalishaji kwenda viwandani.

Akizungumza Mratibu wa Mradi wa C-SDTP, Dkt. Lazaro Kapella, amesema ushiriki wa mradi katika Maonesho ya 88 ni fursa muhimu ya kukutana na wadau mbalimbali, kubadilishana uzoefu, kuonesha teknolojia na ubunifu wa ufugaji wa ng’ombe wa maziwa unaozingatia mabadiliko ya tabianchi, pamoja na kuimarisha ushirikiano katika maendeleo ya tasnia ya maziwa.

Amesema kupitia banda la C-SDTP, wananchi wanapata fursa ya kujifunza kuhusu teknolojia za uzalishaji wa malisho na lishe bora ya mifugo, huduma za afya na uboreshaji wa mifugo, ubora na usalama wa maziwa, uimarishaji wa masoko, huduma za kifedha na uwezeshaji wa vijana na wanawake.

Ameongeza kuwa mradi huo, unaotekelezwa kwa miaka 10 kuanzia 2024 hadi 2034 kwa ushirikiano kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD), unalenga kujenga tasnia ya maziwa yenye tija, shindani, jumuishi na endelevu, ili Tanzania iweze kuongeza uzalishaji na hatimaye kuuza maziwa katika masoko ya nje.




📍Nzuguni : Dodoma

Waziri wa Kilimo, Mh.Daniel Chongolo, ameipongeza Tume ya Taifa ya Umwagiliaji (NIRC) na kuitaka kuhakikisha pampu za Umwagiliaji zilizotengwa kwa ajili ya wakulima zinagaiwa kuanzia Agosti 30 kwa wanufaika katika mikoa husika ili ziweze kutumika kuongeza uzalishaji wa mazao.

Chongolo ametoa maelekezo hayo leo alipotembelea banda la Tume ya Taifa ya Umwagiliaji katika Maonesho ya Wakulima (Nane Nane) yanayoendelea katika viwanja vya John Malechela, Nzuguni, mkoani Dodoma.

Amesema Serikali imeendelea kuwekeza katika upatikanaji wa teknolojia za Umwagiliaji kwa lengo la kuongeza tija ya uzalishaji, hivyo ni muhimu vifaa hivyo viwafikie wakulima kwa wakati ili viweze kutoa matokeo yaliyokusudiwa.

Waziri Chongolo amepongeza jitihada za Tume katika kuratibu na kusimamia utekelezaji wa programu mbalimbali za Umwagiliaji nchini, zikiwemo usambazaji wa pampu na utekelezaji wa miradi ya Umwagiliaji inayolenga kuwawezesha wakulima kuzalisha kwa ufanisi mwaka mzima.

Kwa upande wake, Salome Mallamia Mkurugenzi wa Uendeshaji wa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji ameeleza kuwa Tume itaendelea kutekeleza maelekezo ya Serikali kwa kuhakikisha pampu hizo zinawafikia wakulima watakao nufaika ndani ya muda uliopangwa, hatua itakayochochea ongezeko la uzalishaji, kuinua kipato cha wakulima na kuendelea kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kupitia kaulimbiu ya “Tambua Soko, Ongeza Tija, Kutekeleza Dira 2050.














Top News