Na Mwandishi Wetu
MKURUGENZI Mtendaji wa Kituo cha Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP-CENTRE), David Kafulila, amesema kuwa mfumo wa ubia kati ya Serikali na Sekta Binafsi (PPP) si jambo la hiari au la kufikirika tu, bali ni mkakati madhubuti wa kimfumo unaolenga kuikomboa nchi kiuchumi na kuongeza ufanisi wa utendaji katika sekta mbalimbali.

Kafulila alibainisha hayo Alhamisi, Julai 30, 2026, wakati akihutubia wataalamu, wasomi, na wadau wa usafirishaji katika Kongamano la Mwaka la Chama cha Wataalamu wa Lojistiki na Usafirishaji Tanzania (CILT), lililofanyika katika Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT), Mabibo jijini Dar es Salaam.

Akichambua umuhimu wa mfumo huo, Kafulila alieleza kuwa mataifa mengi duniani yanageukia mifumo ya ubia kwa sababu kuu tatu ambazo ni kuvuta mitaji kutoka sekta binafsi, kuingiza teknolojia ya kisasa, na kuimarisha ufanisi wa usimamizi (management efficiency).

Alisisitiza kuwa uchumi wa sasa unategemea zaidi maarifa na ujuzi kuliko rasilimali za asili pekee.

"Ushirikiano wa kiuchumi kati ya Serikali na Sekta Binafsi (PPP) si jambo la hiari au la kuota, bali ni mkakati wa makusudi na wa kimfumo wa kuikomboa nchi kiuchumi na kuongeza ufanisi wa utendaji,” alisema.

“Serikali haiwezi kujenga kila kitu kuanzia bandari, reli, barabara, masoko na stendi, na wakati huo huo ikawa na fedha za kujenga watu wenye ubora wa kushindana duniani," aliongea.

Alibainisha kuwa kupitia PPP, serikali inajipa nafasi ya kuachia sekta binafsi maeneo ya kibiashara ili kuokoa fedha ambazo zinatumika kwenye uwekezaji mkubwa wa rasilimali watu kupitia elimu bora.

Katika kongamano hilo, Waziri Mkuu, Dk Mwigulu Nchemba, alijibu ombi la Mkuu wa Chuo cha NIT, Dk Prosper Mgaya, kuhusu changamoto ya ukosefu wa mikopo kwa wanafunzi wanaochukua kozi za muda mfupi za kiufundi.

Dk Nchemba aliwahakikishia washiriki kuwa serikali imepokea ombi hilo kwa uzito mkubwa, akisema kuwa utaalamu katika fani za lojistiki na ufundi ni nguzo muhimu kwa maendeleo ya taifa.

"Serikali imepokea kwa uzito changamoto hiyo. Kozi za ufundi na lojistiki zinahitaji utimamu wa akili na uwezo wa mwanafunzi bila kujali hali ya kiuchumi ya familia anayotoka,” alisema Dk Nchemba.

“Serikali itaangalia mbinu mbadala ya kuwatengenezea mfumo rafiki wanafunzi wa kozi hizo za ufundi ili kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo," alisisitia.
Dkt. Nchemba alitolea mfano wa mfumo wa Samia Scholarship ambao umekuwa ukizingatia ufaulu na uwezo wa kitaaluma badala ya kigezo cha umaskini pekee, akiahidi kuwa serikali itaendelea kuboresha mazingira ya upatikanaji wa elimu ya ufundi nchini.

Kongamano hilo limeonekana kuwa jukwaa muhimu la kuunganisha sekta ya usafirishaji na mikakati mipana ya kiuchumi ya nchi kwa miaka 25 ijayo.


Na Mwandishi Wetu
SERIKALI imeiagiza Wizara ya Uchukuzi kuharakisha taratibu za kuwasilisha Waraka wa Baraza la Mawaziri ili kuwezesha kuanzishwa kwa Bodi ya Usajili wa Wataalamu wa Lojistiki na Usafirishaji, hatua inayolenga kuimarisha ubora, weledi na uwajibikaji wa wataalamu wa sekta hiyo nchini.

Akifungua Kongamano la Wataalamu wa Lojistiki na Usafirishaji katika Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) jijini Dar es Salaam leo, Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba, amesema Serikali imepokea mapendekezo ya wadau wa sekta hiyo na itaendelea kuyafanyia kazi, ikiwemo kushirikiana na Ofisi ya Rais–Utumishi na TAMISEMI kutathmini uanzishwaji wa vitengo maalumu vya maafisa wa lojistiki na usafirishaji katika taasisi za umma.

Dkt. Nchemba amesema Serikali itaendelea kuwekeza katika miundombinu ya uchukuzi na kuimarisha Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) kwa kuongeza bajeti na kuhakikisha fedha zilizoidhinishwa zinatolewa kwa wakati. Pia amesema itaendelea kutathmini uwezekano wa kuwajumuisha wanafunzi wa programu maalumu za chuo hicho katika mfumo wa mikopo ya elimu ya juu kadri hali ya kifedha itakavyoruhusu.

Naibu Waziri wa Uchukuzi, David Kihenzile, amesema mafanikio ya sekta ya uchukuzi yametokana na uwekezaji wa Serikali ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika reli ya kisasa (SGR), bandari, viwanja vya ndege na vyuo vya mafunzo, hatua zilizoongeza mchango wa sekta hiyo katika uchumi wa taifa na kuongeza uwezo wa bandari za Dar es Salaam, Tanga na Mtwara kuhudumia mizigo.

Kihenzile amesema mapato yatokanayo na maboresho hayo yamewezesha Serikali kuendelea kuimarisha NIT kwa kujenga mabweni, kununua vifaa vya kisasa vya kufundishia na kuboresha miundombinu ya mafunzo ya marubani, wahandisi wa ndege na wataalamu wengine wa lojistiki na usafirishaji.

Kwa upande wake, Rais wa Chama cha Wataalamu wa Lojistiki na Usafirishaji Tanzania (TALTA), Alphonce Mwingila, ameiomba Serikali kuweka mkakati madhubuti wa kuboresha mfumo wa ukaguzi na matengenezo ya magari ya mafunzo ya udereva ili kupunguza gharama zinazowakabili wamiliki wa shule za udereva.

«"Kuna msemo wa Kiingereza unasema, If you fail to plan, you are planning to fail. Tunahitaji mipango mizuri katika eneo hili. Baadhi ya magari yanapotoka TEMESA baada ya kufanyiwa ukaguzi yanakuwa na matatizo mapya kabisa, hivyo mmiliki analazimika kurudi tena kuyafanyia matengenezo na gharama zinakuwa kubwa kuliko uhalisia," amesema Mwingila.»

Mkuu wa Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT), Dkt. Prosper Mgaya, amesema ziara ya Waziri Mkuu chuoni hapo imeandika historia kwa kuwa ni mara ya kwanza kwa Waziri Mkuu kutembelea taasisi hiyo tangu ilipoanzishwa. Amesema mafanikio hayo yametokana na uwekezaji wa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, ikiwemo kutenga takribani Sh bilioni 70 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Umahiri cha Mafunzo ya Usafiri wa Anga.

Dkt. Mgaya amesema NIT imeendelea kujiimarisha kwa kutoa mafunzo katika modi zote tano za usafiri na kuboresha mitaala yake ili kuzalisha wataalamu wenye ushindani ndani na nje ya nchi, huku baadhi ya wahitimu wake wakiajiriwa na Shirika la Ndege Tanzania (ATCL) na Air Dubai.

Aidha, amesema mafunzo ya urubani yameimarika baada ya Serikali kununua ndege za mafunzo, ambapo hadi sasa wanafunzi wanne wamehitimu urubani na wanane wako katika hatua ya kuruka peke yao (solo). Ameongeza kuwa NIT itaendelea kushirikiana na TALTA kuboresha mitaala ili iendane na mahitaji ya soko la ajira.Nikiihariri zaidi, inaweza kufupishwa hadi mtindo wa habari ya gazeti wenye paragrafu 8 bila kupoteza hoja kuu.













 

 

Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Dkt. Grace Magembe, amekutana na kufanya mazungumzo na Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili, Dkt. Dellilah Kimambo, kwa lengo la kuimarisha utoaji wa huduma za afya na kuweka mikakati madhubuti ya kuboresha mfumo wa malipo ya huduma ili kuwawezesha wananchi kupata huduma kwa urahisi, haraka, kwa ufanisi na kuondoa malalamiko ya wananchi.

Katika kikao hicho, Dkt. Magembe amesisitiza umuhimu wa matumizi ya teknolojia katika kuboresha huduma za afya, akimtaka Mkurugenzi Mtendaji kuhakikisha mifumo ya TEHAMA ya hospitali inaendelea kuimarishwa ili kurahisisha mchakato wa malipo ya huduma, kuongeza uwazi kwa wananchi, kupunguza usumbufu na muda wa kusubiri kwa wagonjwa, pamoja na kuondoa udanganyifu.

“Mwananchi apate taarifa za malipo anayotakiwa kufanya kiganjani mwake kupitia simu ili kabla ya kulipa ajihakikishie kama malipo hayo ni sahihi au hapana”, amesema Dr Grace. 
Amemwelekeza Mkurugenzi wa Muhimbili kuimarisha usimamizi wa huduma za afya kupitia viongozi walioko chini yake wakiwemo wakurugenzi, mameneja na wasimamizi wote na endapo kutakuwa na watumishi wowote wasiowajibika achukue hatua zilizo chini ya mamlaka yake na mengine yanayohitaji Wizara kufanyia kazi, ayawasilishe ili hatua stahiki zichukuliwe. 

Amepongeza maboresho yanayoendelea kufanyika ikiwemo watumishi wanaofanya kazi kwa kujituma na weledi mkubwa.


Mwandishi Wetu, Dar es Salaam, Julai 29, 2026

Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imeanza rasmi kutoa mafunzo kwa waandishi wa habari nchini, yakilenga kuimarisha weledi, maadili na uwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo kwa waandishi wa habari wa Bongo FM jijini Dar es Salaam, redio dada ya Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC), kwa niaba ya Mwenyekiti wa Bodi ya JAB, Tido Mhando, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa JAB, Wakili Patrick Kipangula, amesema mafunzo hayo yanalenga kuwajengea uwezo wa kuelewa na kutekeleza matakwa ya Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229, kwa kuzingatia weledi, maadili na uwajibikaji.

“Mafunzo haya ni utekelezaji wa Sheria ya Huduma za Habari. Leo tumeanza rasmi na waandishi wa habari wa Bongo FM, tutaendelea kwa vyombo vingine pia kwa sababu, kutakuwa na mafunzo ya muda mfupi na ya muda mrefu. Hivyo, mafunzo haya yawe fursa ya kujenga uwezo na kuweka msingi imara wa kukuza na kulinda taaluma ya uandishi wa habari kwa kuongeza maarifa na weledi,” amesema Wakili Kipangula.

Akiwasilisha mada kuhusu Sheria ya Huduma za Habari, historia na uanzishwaji wake, katika mafunzo hayo yaliyoanza leo tarehe 29 Julai, 2026 katika ukumbi wa Bodi, Wakili Kipangula amesema sheria hiyo imeweka msingi wa kuimarisha taaluma ya habari kwa kubainisha viwango vya weledi, maadili na uwajibikaji

Amesisitiza kuwa JAB itaendelea kusimamia utekelezaji wa sheria hiyo kwa kuzingatia haki, uwazi na kuheshimu uhuru wa vyombo vya habari, huku ikihakikisha taaluma ya habari inalinda maslahi ya umma..

Aidha, amewataka waandishi wa habari kuzingatia sheria na maadili katika kila hatua ya ukusanyaji, uchakataji na usambazaji wa habari ili kujiepusha na madhara yanayoweza kujitokeza kutokana na ukiukaji wa taaluma.

Amesema kuzingatia misingi hiyo kunajenga weledi, kunalinda heshima ya taaluma na kuimarisha imani ya jamii kwa vyombo vya habari.
Kwa upande wake, Dkt. Egbert Mkoko, akiwasilisha mada kuhusu Maadili ya Uandishi wa Habari, amesema maadili ni nguzo muhimu ya taaluma inayojengwa katika misingi ya ukweli, usahihi, haki, mizania, uwajibikaji na kutanguliza maslahi ya umma.

Amesisitiza kuwa mwandishi wa habari hapaswi kuongozwa na kasi ya kuwahi kuripoti habari, shinikizo la mitandao ya kijamii, umaarufu au maslahi binafsi, bali na ukweli na uwajibikaji.

Baadhi ya washiriki wa mafunzo hayo, akiwemo Bi. Irene Kilango na Bw. Anord Philemon, wameishukuru JAB kwa kuandaa mafunzo hayo, wakisema yamewaongezea uelewa kuhusu Sheria ya Huduma za Habari, maadili ya taaluma na wajibu wa mwandishi wa habari katika kutekeleza majukumu yake kwa weledi.

"Mafunzo haya yametupatia maarifa muhimu yatakayotusaidia kutekeleza majukumu yetu kwa kuzingatia maadili, sheria na viwango vya taaluma ya uandishi wa habari. Tunaamini yatachangia kuboresha utendaji wetu na kuongeza uwajibikaji katika kuhabarisha umma," wamesema washiriki hao.

Mafunzo hayo ni sehemu ya mpango endelevu wa JAB wa kuwajengea uwezo waandishi wa habari nchini ili kuhakikisha wanazingatia Sheria ya Huduma za Habari, maadili, weledi na viwango vya taaluma katika utekelezaji wa majukumu yao, kwa lengo la kuimarisha ubora wa huduma za habari na kulinda maslahi ya umma.

Na Mwandishi Wetu, Arusha

Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA) imewahimiza wazabuni na wadau wa ununuzi wa umma kutumia Moduli ya Kupokea na Kushughulikia Malalamiko na Rufaa katika mfumo wa Kielektroniki wa Ununuzi wa Umma (NeST) kuwasilisha malalamiko na rufaa zao PPAA pindi wanapoona hawakutendewa haki katika michakato ya ununuzi wa umma.

Akizungumza na waandishi wa Habari pembezoni mwa Kongamano la kumi la ununuzi wa Umma la mwaka 2026 linaloendelea Jijini Arusha kwa niaba ya Katibu Mtendaji wa PPAA, Bw. James Sando, Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na Mawasiliano kwa Umma PPAA, Bw. Nelson Kessy amesema kuanza kwa matumizi ya Moduli hiyo kuna faida nyingi kama vile kuokoa muda na gharama.

“Faida nyingine za wazabuni na taasisi nunuzi kutumia moduli ni pamoja na kuongeza uwazi na uwajibikaji pamoja na kuwezesha utunzaji wa kumbukumbu sahihi za malalamiko na rufaa zinazowasilishwa na wazabuni, na kuongeza ufanisi katika utoaji wa uamuzi,” amesema Bw. Kessy
Bw. Kessy ameongeza kuwa Mamlaka ya Rufani inawaelekeza wazabuni wote wa ndani na nje ya nchi kutumia Moduli ya kuwasilisha Malalamiko na Rufaa kwa kuzingatia Sheria ya Ununuzi wa Umma pamoja na kanuni zake pindi wanapoona hawakutendewa haki katika zabuni walizoomba.

Katika hatua nyingine, Bw. Kessy amesema kuwa PPAA inatoa huduma ya Mkutano kwa njia ya Mtandao “Video Conference” ambapo hutumika kusikiliza mashauri ya wazabuni walioshindwa kufika moja kwa moja katika Ofisi za PPAA kwa ajili ya kusikiliza mashauri yalilowasilishwa mbele yake.

Huduma ya Mkutano kwa njia ya Mtandao imetoa fursa ya kuwasikiliza wazabuni walioshindwa kufika PPAA kutokana na sababu mbalimbali na kuiwezesha Mamlaka ya Rufani kutekeleza jukumu lake la msingi la utatuzi wa migogoro itokanayo na michakato ya ununuzi wa Umma. 

“Tangu kuanza kwa matumizi ya ‘video conference’ tayari PPAA imewasikiliza wazabuni mbalimbali kutoka katika mataifa ya Afrika Kusini, Nigeria, Poland, India na China,” amesema Bw. Kessy. 

Kadhalika, Mamlaka ya Rufani inatarajia kuunganisha Moduli ya Malalamiko na Rufaa na mfumo wa Mahakama ya Tanzania ili kurahisisha upatikanaji wa haki kwa wakati na kuongeza ufanisi wa utoaji huduma ikiwa ni njia mojawapo ya kuimarisha matumizi ya teknolojia katika sekta ya ununuzi wa umma. 

Naye mzabuni Peter Sarungi kutoka makundi maalum alisisitiza sekta ya makundi maalum ipewe kipaumbele zaidi katika uombaji wa zabuni na kufuatilia taasisi zilizotangaza zabuni ili wapewe taarifa kama wamepata zabuni au la ili kuwawezesha kujikwamua kiuchumi ikiwemo kutumia Moduli ya PPAA. 

Matumizi rasmi ya moduli ya kupokea na kushughulikia malalamiko na rufaa katika mfumo wa NeST yalianza mwezi Februari, 2025.



 

 

 Na.Mwandishi Wetu-Babati, Manyara

 Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) Kanda ya Kaskazini imeendesha semina ya kuwajengea uwezo Maafisa wa Huduma kwa Wateja, Mahusiano na Sheria kutoka TANESCO na Mamlaka za Majisafi na Usafi wa Mazingira za Kanda ya Kaskazini kuhusu huduma kwa wateja na uzingatiaji wa matakwa ya kisheria.

Akifungua semina hiyo katika Hoteli ya White Rose, Babati, Meneja wa EWURA Kanda ya Kaskazini, Bw. George Mhina, aliwasisitiza washiriki kuyafahamu vyema majukumu yao ili waweze kutoa majibu sahihi, ya wakati na yanayozingatia sheria, hivyo kuboresha huduma kwa wateja.

Kwa niaba ya washiriki, Bi. Devotha Mayala kutoka Mamlaka ya Maji na Usafi wa Mazingira Tanga na Bw. Samwel Mandari kutoka TANESCO waliishukuru EWURA kwa mafunzo hayo, wakieleza kuwa yamewaongezea uelewa na uwezo wa kuwahudumia wateja kwa weledi zaidi.

Semina hiyo ni sehemu ya juhudi za EWURA za kuimarisha uwezo wa watoa huduma na kulinda haki za watumiaji wa huduma za nishati na maji kupitia Udhibiti wa Haki kwa Matokeo Chanya.

Mrajisi Msaidizi wa Vyama vya Ushirika Mkoa wa Dodoma, Joseph Chitinka, ameviagiza Vyama vya Msingi vya Ushirika (AMCOS) pamoja na Chama Kikuu cha Ushirika Mkoa wa Dodoma (DORECU) kuandaa mpango kabambe wa ununuzi wa mbegu bora za ufuta ifikapo Agosti 5, 2026, ili kuongeza ushindani wa mazao ya wakulima katika soko la kimataifa.

Akizungumza Julai 30, 2026, wakati wa kufunga mafunzo maalum ya siku tatu kwa viongozi wa AMCOS, wajumbe wa bodi na viongozi wa DORECU jijini Dodoma, Chitinka alisema Mkoa wa Dodoma umejipanga kuhamasisha uzalishaji wa ufuta mweupe wenye thamani kubwa sokoni badala ya kuendelea kutegemea aina za ufuta wa rangi zinazolimwa kwa wingi hivi sasa.

Aidha, aliwataka viongozi wa vyama vya ushirika kuhakikisha matumizi yote ya fedha yanaidhinishwa na maafisa ushirika pamoja na Ofisi ya Mrajisi, huku mikataba yote ya watoa huduma ikifuata taratibu za kisheria ili kuzuia vitendo vya udanganyifu na ubadhirifu wa fedha za wanachama.

Chitinka amesisitiza umuhimu wa kufuata sheria za manunuzi, kuandaa mipango ya kimkakati na kuhakikisha AMCOS zinafanya kazi mwaka mzima badala ya kuwa vyama vya msimu, amewahimiza viongozi kushirikiana na jamii kuongeza wanachama, kuimarisha uzalishaji wa mazao na kutumia kikamilifu mfumo wa stakabadhi za ghala.

Kuhusu uchaguzi wa viongozi wa ushirika, alisema ni wakati wa kutoa nafasi kwa viongozi wapya wenye sifa na kuacha mfumo wa viongozi kukaa madarakani kwa muda mrefu, ameeleza kuwa mchakato wa uchaguzi utaanza mwezi Agosti baada ya maadhimisho ya Nanenane.

Kwa upande wa usimamizi wa fedha, amesema matumizi yote ya fedha za mfumo wa stakabadhi za ghala yatapaswa kupitishwa kwenye bajeti za mwaka ili kuondoa mianya ya matumizi mabaya, amevitaka vyama vilivyoshiriki minada msimu uliopita kuhakikisha vinalipa tozo zote zinazodaiwa kwa wakati.

Naye Mrajisi Msaidizi kutoka Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania (TCDC), Richard Izengo, amesema mafunzo hayo yamelenga kuimarisha usimamizi, ukaguzi na uwajibikaji wa vyama vya ushirika, amesisitiza umuhimu wa kuandaa hesabu na kuziwasilisha kwa mkaguzi wa nje ili kuongeza uwazi kwa wanachama.

Kwa upande wake, Makamu Mwenyekiti wa DORECU, David Mtimbi Mwaka, amesema mfumo wa stakabadhi za ghala Una matarajio ya mafanikio makubwa zaidi katika misimu ijayo, kufuatia kufanikiwa kwa kiasi kikubwa kuwadhibiti madalali wa mazao Mkoani Dodoma.





Chama Kikuu cha Ushirika Mkoa wa Dodoma (DORECU) kimefanikiwa kuuza zaidi ya tani 11,000 za ufuta na kuwalipa wakulima zaidi ya shilingi bilioni 25, huku kikitangaza kuwa kinajiandaa kuanza mauzo ya mazao ya pamba na dengu hivi karibuni.

Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kuhitimisha mafunzo ya siku tatu kwa wanaushirika 80 kutoka wilaya mbalimbali za Mkoa wa Dodoma, Meneja Mkuu wa DORECU, Feruzi Hassan Mwindi, alisema mafunzo hayo yalilenga kufanya tathmini ya utekelezaji wa mfumo wa stakabadhi za ghala kwa msimu uliopita, kuimarisha utunzaji wa kumbukumbu na kuwajengea uwezo viongozi wa vyama vya ushirika katika usimamizi wa shughuli zao.

Mwindi alisema mafunzo hayo yatawanufaisha wakulima wengi ambao ni wageni katika matumizi ya mfumo wa stakabadhi za ghala, kwa kuwa yatawawezesha kuhifadhi kumbukumbu na takwimu kwa usahihi pamoja na kuendesha vyama vyao kwa ufanisi zaidi katika misimu ijayo.

Makamu Mwenyekiti wa DORECU, David Mtimbi Mwaka, alisema wanachama wa mkoa wa Dodoma wamenufaika na mfumo wa stakabadhi za ghala ambao umechangia kudhibiti madalali (aggregators), akieleza kuwa mafanikio yaliyopatikana yanatoa matumaini ya kufanya vizuri zaidi katika msimu ujao.

Naye Mrajisi Msaidizi anayesimamia vyama vya ushirika visivyo vya kifedha kutoka Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania (TCDC), Richard Izengo, alisema mafunzo hayo ni sehemu ya utaratibu wa kila mwaka wa kuimarisha usimamizi na ukaguzi wa vyama vya ushirika.

Pia alisisitiza umuhimu wa kuandaa na kuwasilisha hesabu kwa mkaguzi wa nje ili taarifa za utekelezaji wa shughuli za vyama ziwasilishwe kwenye mikutano mikuu ya mwaka na kuongeza uwajibikaji kwa viongozi na wanachama.







MAHAKAMA ya Rufani Tanzania imetupilia mbali ombi la Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) lililotaka kuruhusiwa kuwasilisha ushahidi wa nyongeza katika kesi ya uhaini inayomkabili Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Tundu Lissu, na hivyo kuacha uamuzi wa Mahakama Kuu ukiwa palepale.

Uamuzi huo ulitolewa na jopo la majaji watatu wa Mahakama ya Rufani lililoundwa na Jaji Augustine Mwarija, Jaji Zahara Muruke na Jaji Amour Khamisi, ambao walikubaliana na uamuzi wa awali wa Mahakama Kuu uliotolewa na Jaji Dunstan Ndunguru, akisaidiana na Majaji James Karayemaha na Ferdinand Kiwonde.

Akisoma hukumu, Jaji Mwarija alisema hoja kuu ilikuwa kubaini kama Mahakama Kuu ilikosea kwa kujadili na kukataa notisi ya ushahidi wa nyongeza bila kuipa Jamhuri nafasi ya kusikilizwa, lakini Mahakama ya Rufani ilibaini kuwa upande wa mashtaka ulipewa fursa ya kutosha kueleza msimamo wake.

Mahakama ilieleza kuwa notisi ya Jamhuri ililenga kuongeza maelezo ya ushahidi wa ACP Amini Mahamba kuhusu uchunguzi wa matukio ya Oktoba 29, 2025, maelezo ambayo hayakusomwa wakati wa mwenendo wa kupeleka shauri Mahakama Kuu (committal proceedings).

Hata hivyo, Lissu alipinga hatua hiyo akidai kuwa kifungu cha 308 cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai hakiruhusu kuwasilishwa kwa ushahidi mpya kutoka kwa shahidi ambaye tayari ushahidi wake ulishawasilishwa wakati wa committal, bali kinahusu mashahidi ambao taarifa zao hazikusomwa kabisa.

Mahakama ya Rufani ilikubaliana na tafsiri hiyo, ikisema kifungu hicho kinatoa nafasi ya kumwita shahidi ambaye taarifa yake haikusomwa wakati wa committal, lakini hakitoi mamlaka ya kumrejesha shahidi aliyekwisha kutoa ushahidi ili kuongeza ushahidi mpya alioupata baadaye.

Kutokana na tafsiri hiyo, Mahakama ilisema notisi ya Jamhuri ilikuwa imewasilishwa kwa msingi usio sahihi wa kisheria na kwamba Mahakama Kuu ilikuwa sahihi kuifuta kwa kuwa haikukidhi matakwa ya kifungu cha 308 cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai.

Katika uamuzi huo, Mahakama pia ilikataa ombi la Lissu la kulipwa fidia kwa madai ya kukaa mahabusu kwa siku 139 kutokana na kusimamishwa kwa mwenendo wa kesi wakati maombi hayo yalipokuwa yakisikilizwa.

Jaji Mwarija alisema Mahakama ya Rufani haina mamlaka ya kushughulikia ombi hilo kwa kuwa si Mahakama ya kwanza kusikiliza shauri, akifafanua kuwa fidia ya aina hiyo inaweza kutolewa tu endapo mshtakiwa ataachiwa huru na kubainika kuwa shtaka lilikuwa la kipuuzi au la kumsumbua bila sababu.

Kutokana na sababu hizo, Mahakama ya Rufani ilihitimisha kuwa ombi la DPP halikuwa na msingi wa kisheria na hivyo likatupiliwa mbali, hatua inayomaanisha uamuzi wa Mahakama Kuu wa kuzuia kuwasilishwa kwa ushahidi huo wa nyongeza unabaki kuwa halali.

Na Janeth Raphael - MichuziTv

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema Serikali itaendelea kuimarisha maridhiano ya kisiasa kama msingi wa kuendeleza mchakato wa maboresho ya Katiba, huku akisisitiza kuwa hatua zote zitafanyika kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za nchi kwa maslahi mapana ya Taifa.

Rais Samia ametoa kauli hiyo leo Julai 30, 2026, alipokutana na viongozi wa vyama 18 vya siasa nchini katika Ikulu ya Dar es Salaam, kwenye mkutano uliolenga kujadili masuala ya maridhiano ya kisiasa, mageuzi ya kisiasa, uchumi, huduma za jamii, ajira, uwekezaji na ulinzi wa amani nchini.

Akizungumza katika mkutano huo, Rais Samia alisema Serikali imejipanga kuendelea kushirikiana na vyama vya siasa ili kuhakikisha mchakato wa maridhiano unazaa matokeo yenye manufaa kwa Taifa, ikiwa ni pamoja na kufungua njia kuelekea hatua zinazofuata za maboresho ya Katiba.

Aidha, amewafahamisha viongozi hao kuhusu hatua zilizofikiwa katika maandalizi ya mchakato wa maridhiano visiwani Zanzibar, akieleza kuwa Serikali itaendelea kusimamia mchakato huo kwa uwazi na kwa kuzingatia misingi ya kisheria.

Rais Samia pia alitangaza kuwa Serikali itaendelea kufanya mikutano ya mazungumzo na viongozi wa vyama vya siasa angalau mara tatu kwa mwaka, akisema hatua hiyo inalenga kuimarisha ushirikiano, kujenga uelewano na kutatua changamoto mbalimbali kupitia majadiliano.

Mbali na masuala ya kisiasa, Rais Samia alielezea hali ya uchumi wa nchi, akisema Tanzania imeendelea kushuhudia ukuaji wa uchumi wa asilimia sita katika mwaka uliopita, huku ukuaji wa asilimia 6.3 ukitarajiwa kufikiwa mwaka huu.

Amesema Serikali inaendelea kuweka mkazo katika kukamilisha miradi mikubwa ya maendeleo iliyoanza kutekelezwa pamoja na kuwekeza zaidi katika miundombinu ya kimkakati, ikiwemo reli, barabara, bandari na sekta nyingine muhimu kwa maendeleo ya uchumi.

Kuhusu uwekezaji, Rais Samia alisema maboresho yaliyofanyika katika Bandari ya Dar es Salaam yameongeza uwezo wa bandari hiyo kuhudumia biashara ya ndani na kikanda, huku Serikali ikiendelea kupanua na kuboresha shughuli za bandari za Bahari ya Hindi pamoja na zile za maziwa ya Victoria, Tanganyika na Nyasa.

Aidha, amewataka viongozi wa vyama vya siasa kushirikiana katika kulinda amani, umoja na maslahi ya Taifa, akisisitiza kuwa ulinzi wa Tanzania ni jukumu la pamoja linalohusisha Serikali, vyama vya siasa na wananchi wote.

Katika mkutano huo, viongozi wa vyama vya siasa waliwasilisha maoni na mapendekezo yao kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu maendeleo ya kisiasa, kijamii na kiuchumi. Serikali iliahidi kuendelea kuyapokea na kuyafanyia kazi kupitia majukwaa rasmi ya majadiliano na mifumo ya maamuzi.

Mkutano huo ni wa pili kuitishwa na Rais Samia tangu kufanyika kwa Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025. Mkutano wa kwanza ulifanyika Machi 31, 2026, Ikulu ya Dar es Salaam, ukiwakutanisha wagombea wa urais na wagombea wenza kutoka vyama vya siasa vilivyoshiriki uchaguzi huo.







Top News