Na Mwandishi Wetu
MKUU wa Shughuli za serikali (Chief of Staff) wa Ghana Dkt Julius Debras ametoa wito kwa nchi za Afrika kuangalia kwa namna gani rasilimali zilizopo zinaweza kujitosheleza kama bara hususani katika sekta ya nishati.

Dkt Debras ametoa wito huo katika wiki ya mafuta Afrika inayoendelea Accra Ghana wakati wa hotuba yake akimwakilisha Rais wa nchi hiyo John Dramani Mahama.

Amesema kuwa endapo bara la Afrika litakuwa na nishati ya uhakika itasaidia kuinua uchumi lakini swala la ajira pia halitakuwa wimbo kwani kutakuwa na maendeleo ya uhakika ya viwanda.

Ameweka bayana kuwa kwa upande wa Mkondo wa Juu wa Petroli wa Ghana, serikali imeweka mikakati mathubuti kuhakikisha kupitia sekta hiyo wanapata wawekezaji wenye uhakika.

Amesema ni lazima kama bara la Afrika kuangalia aina ya wawekezaji wanaokuja kuwekeza katika nishati ni lazima wawe na nguvu ya kiuchumi ili kuweza kuleta manufaa ya uhakika na haraka katika sekta hiyo.

Kwa upande wake Kamishna wa Miundombinu na Nishati kutoka Kamisheni ya Umoja wa Afrika Lerato Mataboge amesema vijana wa Afrika wapo tayari katika mabadiliko ya nishati yanayoendelea barani Afrika.

Amesema kinachotakiwa hivi sasa ni mshikamano wa Afrika kuweka njia madhubuti katika kuhakikisha kuwa katika kuelekea maendeleo hayo kuwe na mabadiliko makubwa katika matumizi ya teknolojia kwa kutoa vipaumbele katika bunifu zote zinazofanywa na vijana wa Afrika.

Ameweka bayana kuwa Umoja wa Afrika umeweka utengamano wa viwanda ili kuhakikisha kuwa kunakuwa na ushirikiano wa kikanda katika sekta ya nishati ambao baadaye utaleta tafsiri sahihi ya kuwa na nishati ya uhakika katika bara zima.

Wiki ya Mafuta barani Afrika imeanza Septemba 01 hadi 03 ambapo Tanzania imewakilishwa na wajumbe kutoka Wizara ya Nishati, wajumbe kutoka Mamlaka ya Udhibiti Mkondo wa Juu wa Petroli (PURA), na wajumbe kutoka Mamlaka ya Udhibiti wa Petroli Zanzibar (ZPRA).













Na Janeth Raphael – MichuziTv - Bungeni Dodoma


SERIKALI imesema maandalizi ya Tanzania kuwa mwenyeji wa Mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2027 yanaendelea kwa kasi, huku ikihakikisha miundombinu muhimu ya michezo na huduma wezeshi inakamilishwa kwa wakati.

Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba, amesema hayo leo, Ijumaa, Septemba 4, 2026, jijini Dodoma, wakati akiwasilisha hoja ya kuahirisha Bunge la 13, Mkutano wa Nne.

Amesema kazi zinazoendelea zinahusisha ujenzi na ukarabati wa viwanja vya mashindano na mazoezi, barabara zinazounganisha maeneo ya viwanja, pamoja na kuhakikisha upatikanaji wa huduma muhimu za afya, maji na umeme.

Kwa upande wa viwanja, Dkt. Mwigulu amesema ujenzi wa Uwanja wa Jiji la Arusha umefikia zaidi ya asilimia 91, huku ujenzi wa uwanja mwingine wenye uwezo wa kuchukua zaidi ya watazamaji 32,000 ukiendelea.

Amesema kwa upande wa Dar es Salaam, ukarabati wa Uwanja wa Benjamin Mkapa pamoja na viwanja vya mazoezi umekamilika, hatua inayoongeza utayari wa jiji hilo katika maandalizi ya mashindano hayo.

Kwa upande wa Zanzibar, Serikali imeeleza kuwa Uwanja wa Fumba unaendelea katika hali nzuri, huku miundombinu mingine ikiwemo New Amaan Complex, Amaan Annex One na Annex Two ikiwa imekamilika. Aidha, Uwanja wa Amaan umeelezwa kuwa katika hali nzuri kwa matumizi ya mashindano.

Dkt. Mwigulu amewataka wasimamizi wa miradi kuhakikisha fedha zinazowekezwa katika maandalizi ya AFCON 2027 zinazalisha thamani inayolingana na uwekezaji huo, akisisitiza kuwa Tanzania inapaswa kutumia nafasi ya kuwa mwenyeji wa mashindano hayo kupata manufaa ya kiuchumi.

Amesema wizara na taasisi zinazohusika zinapaswa kuendelea kuratibu mikakati itakayowezesha Tanzania kunufaika kikamilifu na fursa zitakazotokana na uenyeji wa mashindano hayo, huku akiwataka wadau wote kushiriki kikamilifu ili kuepusha vikwazo vinavyoweza kupunguza ufanisi na manufaa yanayotarajiwa.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amesisitiza umuhimu wa Tanzania kuwa na timu ya taifa yenye ushindani wakati wa mashindano hayo, akisema mwenyeji hapaswi kuwa mshiriki wa kawaida au “msindikizaji”.

“Sisi ni wenyeji wa mashindano, hivyo tunapenda kuona timu ya taifa pia inakuwa na ubora na sio msindikizaji,” amesema Dkt. Mwigulu.

Amewataka makocha, Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) na benchi la ufundi kuanza mapema kuweka mikakati maalumu itakayoiwezesha timu ya taifa kufanya vizuri katika AFCON 2027.

Tanzania itakuwa miongoni mwa wenyeji wa AFCON 2027 pamoja na Kenya na Uganda, hali inayoiweka nchi katika nafasi ya kutumia mashindano hayo kukuza sekta ya michezo, utalii, biashara na shughuli nyingine za kiuchumi.


Na Janeth Raphael – MichuziTv, Bungeni Dodoma


WAZIRI Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba, ameiagiza Wizara ya Madini kwa kushirikiana na Wizara ya Fedha pamoja na Ofisi ya Waziri Mkuu–TAMISEMI, kuchukua hatua za haraka kukabiliana na changamoto zinazokwamisha ufanisi wa sekta ya madini, ikiwemo tozo zinazotozwa zaidi ya viwango vilivyoainishwa kisheria.

Dkt. Mwigulu ametoa agizo hilo leo Septemba 4, 2026, wakati akilihutubia Bunge kabla ya kuahirishwa kwa shughuli zake hadi Oktoba 27, 2026, akisisitiza kuwa sekta ya madini imeendelea kuwa miongoni mwa sekta muhimu zinazochangia kwa kiasi kikubwa katika ukuaji wa uchumi na mapato ya Taifa.

Amesema mafanikio yaliyopatikana katika sekta hiyo yamechangiwa kwa kiasi kikubwa na mageuzi yanayoendelea kufanywa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan, pamoja na ushiriki wa wadau mbalimbali wa sekta ya madini.

“Sekta ya madini imekuwa moja ya sekta kinara inayochangia katika mapato ya Taifa,” amesema Dkt. Mwigulu.

Amesema pamoja na mchango wa wachimbaji wakubwa, wachimbaji wadogo wameendelea kuongeza uzalishaji wa madini siku hadi siku, hali ambayo imechangiwa na juhudi za Serikali katika kuweka mazingira wezeshi kwa Watanzania kushiriki na kunufaika na rasilimali hizo.

Hata hivyo, Dkt. Mwigulu amesema Serikali inatambua kuwa bado kuna changamoto zinazohitaji kushughulikiwa ili kuongeza ufanisi wa sekta hiyo, akitaja miongoni mwa changamoto hizo kuwa ni baadhi ya tozo zinazowatozwa wachimbaji wa madini katika maeneo mbalimbali.

Amesema baadhi ya tozo hizo zinahusisha malipo ya huduma yanayozidi kiwango kilichoainishwa katika Sheria ya Madini, hali ambayo imekuwa ikileta malalamiko miongoni mwa wachimbaji.

“Kwa mujibu wa sheria, kuna viwango vilivyowekwa. Hivyo, niwaelekeze Wizara ya Madini pamoja na Wizara ya Fedha na Ofisi ya Waziri Mkuu–TAMISEMI wakae kwa haraka kuziangalia changamoto hizo,” amesema.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu ameitaka Wizara ya Madini kuchukua hatua kali kwa watu wanaoshikilia leseni za uchimbaji kwa muda mrefu bila kuendeleza maeneo waliyopewa, akisema hali hiyo inawanyima Watanzania wengine, hususan vijana na wachimbaji wadogo, fursa ya kushiriki katika shughuli za uchimbaji.

Amesema kushikilia leseni bila kuendeleza maeneo husika ni kinyume na matakwa ya sheria na kwamba Serikali haiwezi kuruhusu maeneo yenye rasilimali kubaki bila kuzalisha huku wananchi wengine wakikosa fursa za kuyatumia.

“Yeyote anayetaka leseni yake isifutwe, atimize masharti yaliyowekwa kwenye leseni, aiendeleze na awape nafasi vijana wengine wa Kitanzania kufanya shughuli za uchimbaji,” amesisitiza.

Dkt. Mwigulu amemwelekeza Waziri wa Madini kuchukua hatua za kisheria, ikiwemo kufuta vibali na leseni za wale watakaokiuka masharti na kugawa upya maeneo hayo kwa Watanzania wenye uwezo na nia ya kuyaendeleza.

Amesema hatua kama hizo tayari zimewahi kuchukuliwa na Rais Samia katika maeneo mbalimbali nchini, ambapo leseni zilizoshikiliwa bila kuendelezwa zilifutwa na maeneo hayo kupewa waombaji wengine.

Waziri Mkuu, amesema hatua hizo zimekuwa miongoni mwa sababu zilizochangia kuongezeka kwa uzalishaji, mapato na mchango wa sekta ya madini katika uchumi wa Taifa.

Amesema Serikali itaendelea kusimamia sekta hiyo kwa kuhakikisha rasilimali za madini zinatumika ipasavyo na kutoa manufaa kwa Taifa pamoja na kutoa fursa kwa Watanzania, hususan vijana na wachimbaji wadogo, kushiriki kikamilifu katika shughuli za uchimbaji.



Na Janeth Raphael - MichuziTv 

MAMLAKA ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) imeendelea kuimarisha mafunzo yanayolenga kuwaandaa Watanzania wenye ujuzi unaoendana na mahitaji ya sekta ya madini, ikiwemo teknolojia za kisasa zinazotumika katika uchimbaji na uchakataji wa madini.

Mkurugenzi Mkuu wa VETA, CPA Anthony Kasore, amesema sekta ya madini ni miongoni mwa sekta muhimu katika uchumi wa Tanzania kutokana na mchango wake katika pato la Taifa, uwekezaji, ajira pamoja na maendeleo ya viwanda vinavyoongeza thamani ya rasilimali za nchi.

Akizungumza na wanahabari jijini Dodoma Septemba 4, 2026, Kasore amesema maendeleo ya sekta ya madini hayawezi kutegemea uwepo wa rasilimali pekee, bali yanahitaji pia wataalamu wenye uwezo wa kutumia, kutengeneza na kusimamia teknolojia na mitambo inayotumika katika migodi ya kisasa.

Amesema kwa kutambua umuhimu wa kujenga nguvu kazi yenye ujuzi katika sekta hiyo, mwaka 2008 VETA kwa kushirikiana na Chemba ya Migodi Tanzania (TCM) ilianzisha Programu ya Mafunzo ya Ufundi kwa Shughuli za Uchimbaji Madini (Integrated Mining Technical Training - IMTT) katika Chuo cha VETA Moshi.

Kupitia programu hiyo, VETA imekuwa ikitoa mafunzo katika fani mbalimbali zinazohitajika kwenye sekta ya madini, zikiwemo Heavy Moving Equipment Mechanics, Fitting and Machining, Plater Welding, Auto Electrical na Industrial Electrical Installation.

 Kasore,amesema tangu kuanzishwa kwa programu hiyo, zaidi ya vijana 1,688 wamepata mafunzo huku jumla ya kampuni 17 zikishiriki katika utekelezaji wa programu hiyo.

Hata hivyo, amesema mabadiliko ya teknolojia katika sekta ya madini yamelazimu VETA kuendelea kuboresha mafunzo yake ili kuhakikisha ujuzi unaotolewa unaendana na mahitaji halisi ya migodi ya kisasa, hususan matumizi ya mitambo ya uchimbaji chini ya ardhi.

Katika hatua hiyo, VETA kwa kushirikiana na TCM imeandaa mitaala sita mipya ya mafunzo ya uchimbaji madini chini ya ardhi, ambayo inalenga kuwaandaa vijana katika matumizi na uendeshaji wa vifaa na mitambo ya kisasa.

Mitaala hiyo inahusisha Bogger Equipment Operation, Jumbo Equipment Operation, Long Hole Drill Rig, Cubex (ITH) Equipment Operation, Underground Charge-Up Operation pamoja na Lifting and Rigging Operations.

Kasore amesema mafunzo hayo yanalenga kuhakikisha kuwa ukuaji wa sekta ya madini unatoa nafasi kubwa zaidi kwa Watanzania wenye ujuzi kushiriki katika shughuli mbalimbali za uchimbaji, huku wakinufaika na fursa za ajira zinazotokana na maendeleo ya sekta hiyo.

Aidha, VETA inaendelea kutekeleza Mradi wa Madini Muhimu (Critical Minerals Project) kwa kushirikiana na taasisi za GTK na REDU Edu kutoka Finland, pamoja na ASNL ya Tanzania inayowakilisha sekta binafsi.

Mradi huo unatarajiwa kuwafikia vijana wapatao 400 kupitia mafunzo yanayohusu uchimbaji, uchakataji pamoja na ukuzaji wa mnyororo wa thamani katika sekta ya madini muhimu.

Kasore amesema hatua za awali za mradi huo tayari zimeanza, ambapo wakufunzi 25 wa VETA wamepatiwa mafunzo ya wiki sita nchini Finland na kwa sasa wanaendelea kupata mafunzo katika migodi mbalimbali nchini Tanzania kwa lengo la kuongeza uelewa wa mazingira na mahitaji ya sekta hiyo nchini.

Amesema hatua hiyo ni muhimu katika kujenga uwezo wa VETA kutoa mafunzo yanayokidhi mahitaji mahsusi ya uchimbaji na uchakataji wa madini muhimu, sambamba na kuongeza ushiriki wa Watanzania katika mnyororo wa thamani wa sekta hiyo.

Mkurugenzi huyo amewataka wadau wa sekta ya madini, hususan kampuni za uchimbaji, watengenezaji na wasambazaji wa mitambo na vifaa vya migodini pamoja na taasisi nyingine zinazohusika katika mnyororo wa thamani, kuendelea kushirikiana na VETA katika kuandaa rasilimali watu yenye ujuzi unaohitajika.

Amesema ushirikiano huo utasaidia kuongeza ushiriki wa Watanzania katika sekta ya madini, kuimarisha matumizi ya teknolojia za kisasa na kuhakikisha ukuaji wa sekta hiyo unaendelea kuchangia katika ajira, uzalishaji na maendeleo ya Taifa.





Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Dkt. Jabiri K. Bakari, amethibitisha dhamira ya Mamlaka hiyo ya kujenga Mamlaka ya Usafiri wa Anga ya kiwango cha kimataifa barani Afrika, yenye matarajio ya kufikia viwango vinavyolingana na mamlaka za usafiri wa anga za Ulaya katika ubora wa udhibiti, umahiri wa kitaalamu, ufanisi wa kiutendaji na usimamizi wa usalama wa anga.

Alitoa kauli hiyo wakati wa kikao cha kuhitimisha ujumbe wa wataalamu wa msaada wa kujengeana uwezo kutoka Shirika la Usalama wa Anga la Umoja wa Ulaya (EASA), kilichofanyika tarehe 3 Septemba 2026 katika Makao Makuu ya TCAA jijini Dar es Salaam. Dkt. Bakari aliushukuru Umoja wa Ulaya kwa kuendelea kutoa msaada na kuonyesha imani katika maendeleo ya Tanzania.

 Pia alieleza juhudi zinazofanywa na TCAA kuimarisha mifumo yake ya usimamizi, ikiwemo uundaji na utekelezaji wa Mfumo wake wa ndani wa TCAA wa Huduma za Usafiri wa Anga (Civil Aviation Services Portal – CASP), ambao ulipewa pongezi na timu ya EASA.

Timu ya EASA ilieleza kuridhishwa kwake na maendeleo na juhudi zilizooneshwa na TCAA wakati wa ziara hiyo ya siku tatu. Aidha, timu hiyo ilitambua maendeleo yaliyofikiwa na kuhimiza TCAA kuendeleza kasi katika kushughulikia masuala yote muhimu ya usimamizi wa usalama wa anga.

Kwa upande wake Mkuu wa Ujumbe wa Umoja wa Ulaya alithibitisha dhamira ya EU ya kuendelea kuisaidia Tanzania kupitia msaada wa kitaalamu, mbinu za utekelezaji wa vitendo na kubadilishana ujuzi. Aidha, alieleza kuwa Umoja wa Ulaya umetenga Euro milioni 2 kwa ajili ya msaada unaohusiana na kuboresha zaidi Masuala ya usafiri wa anga nchini.

Ujumbe wa EASA uliongozwa na Bw. Jose Miguel Manso Angulo akiambatana na Bw. Gustavo Juan Roman Barba na Bw. Antonio Portales Pelaez.

Ujumbe huo, uliofika nchini kwa siku tatu kuanzia tarehe 1 hadi 3 Septemba 2026, ulifuatilia maendeleo ya Nchi (State) katika utekelezaji wa hatua za marekebisho pamoja na kuimarisha usimamizi wa usalama wa Usafiri wa anga. 

Majadiliano yalihusu maeneo ya ki sheria, muundo wa taasisi, uchunguzi wa ajali ndege, utoaji wa leseni kwa eneo la rasilimali watu la Usafiri wa anga, ubora wa ndege kwa matumizi (airworthiness) na uendeshaji wa ndege, pamoja na kufanya vikao na waendeshaji wa mashirika ya ndege kuhusu hoja zilizobainishwa, Mipango ya Hatua za Marekebisho (Corrective Action Plans) na ufuatiliaji wa utekelezaji wake.

Ujumbe huo ni sehemu ya juhudi zinazoendelea za Tanzania za kuimarisha usimamizi wa usalama wa Usafiri wa anga na kuonesha maendeleo endelevu kuelekea kutimiza matakwa ya kuondolewa kwenye Orodha ya Usalama wa Anga ya Umoja wa Ulaya (European Union Air Safety List).

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Dkt. Jabiri K. Bakari akizungumza wakati wa kikao cha kuhitimisha ujumbe wa timu wataalam kutoka Shirika la Usalama wa Anga la Umoja wa Ulaya (EASA).




ALAF Limited kwa mara nyingine imeibuka mshindi katika Tuzo za Rais za mzalishaji Bora wa Mwaka (PMAYA), toleo la 19 hii ikiwa ni mara ya 17 mfulululizo tangu ianze kushiriki katika tuzo hizi..

Tuzo hii ya mshindi wa kwanza katika kipengele cha chuma na Bidhaa za chuma, ilikabidhiwa na Makamu wa Rais Mh. Deogratias Ndejembi.Tuzo hizi hutolewa na kuratibiwa na Shirikisho la Viwanda Tanzania (CTI).

“Tuzo hii inadhihirisha uwajibikaji wetu katika kuzalisha katika viwango bora duniani, kuwa mstari wa mbele katika uvumbuzi na kuwa sehemu ya ukuzaji wa viwanda Tanzania,” alisema Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Uhusiano, Hawa Bayumi.

Aliishukuru CTI, timu nzima ya ALAF na kila mteja anayeendelea kujenga pamoja na ALAF. “Asanteni kwa kutuunga mkono na imani yenu kwetu . Pamoja tutaendelea kujenga viwanda imara, jamii imara na Tanzania imara zaidi,” aliongeza.

#ALAFLimited #19thPMAYA


 Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki (Mb), amesema Tanzania inaendelea kuweka mazingira wezeshi ili wananchi wote wapate huduma za mawasiliano zilizo jumuishi, nafuu, salama na zenye uhakika, sambamba na kuimarisha ujuzi wa kidijitali na matumizi yenye tija ya teknolojia.

Waziri Kairuki ameyasema hayo wakati akishiriki Mkutano wa Saba wa Jukwaa la Sera za Mawasiliano na Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (WTPF-26), unaofanyika Nassau, Bahamas, ambapo amesema hatua hizo zinalenga kutekeleza Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 na Mkakati wa Taifa wa Uchumi wa Kidijitali 2024–2034.

Amesema Tanzania imekamilisha ujenzi wa minara 758 ya teknolojia ya 4G, hatua iliyowezesha zaidi ya vijiji 1,400 na takribani wananchi milioni 8.5 waliokuwa hawapati huduma za mawasiliano ya uhakika kuunganishwa na huduma hizo.

Aidha, kupitia Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), Serikali imeanzisha Vilabu vya Kidijitali 800 kwa ajili ya kujenga ujuzi wa TEHAMA, kuwezesha huduma za Wi-Fi katika maeneo 100 ya umma na kujenga maabara za kompyuta katika shule 250 za umma, zikiwemo huduma zinazozingatia mahitaji ya wanafunzi wenye ulemavu.

Akieleza vipaumbele vya Tanzania katika kuziba pengo la kidijitali, Waziri Kairuki amesema nchi inalenga kupanua huduma za mawasiliano kwa gharama nafuu, kuongeza ujuzi wa kidijitali na matumizi ya Akili Unde (AI), pamoja na kuendeleza miundombinu ya kidijitali iliyo salama, jumuishi na inayolinda taarifa binafsi za watumiaji.

Waziri Kairuki amesema Tanzania iko tayari kushirikiana na Umoja wa Kimataifa wa Mawasiliano (ITU) na wadau wengine wa maendeleo kuimarisha ujuzi wa kidijitali na matumizi ya Akili Unde barani Afrika. Amesisitiza kuwa mafanikio ya mageuzi ya kidijitali hayapaswi kupimwa kwa idadi ya minara pekee, bali kwa namna teknolojia inavyoboresha maisha, kuongeza fursa za kiuchumi na kijamii na kuhakikisha hakuna anayebaki nyuma katika uchumi wa kidijitali.


 


KAMPUNI ya Uchimbaji Madini ya Barrick imeeleza kuridhishwa na huduma za kodi zinazotolewa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na kusifu mazingira ya kodi ambayo ni shirikishi kwa wananchi.

Kauli hiyo imetolewa na Meneja Mkazi wa Barrick Gold Mine Tanzania  Melkiory Ngido wakati wa kikao baina ya Uongozi wa Kampuni hiyo na Kamishna Mkuu wa TRA Yusuph Juma Mwenda katika ofisi za TRA jijini Dar es Salaam. 

Ngido amesema utaratibu uliowekwa na TRA wa kufungua milango na kukutana na Walipakodi kujadili masuala mbalimbali ya kikodi umekuwa na tija katika kuongeza uelewa wa kodi na kuhamasisha ulipaji wa kodi kwa hiari. 

"Sisi tumekuwa na utaratibu wa kila mwaka kukutana na Uongozi wa TRA kueleza hali yetu ya kibiashara na namna tutakavyolipa kodi, na kama ambavyo imekuwa kwa vipindi vingine hali yetu kibiashara ni nzuri na tutaendelea kulipa kodi kwa hiari" amesema Ngido. 

Kwa upande wake Kamishna Mkuu wa TRA Yusuph Juma Mwenda amesema Mamlaka hiyo itaendelea kuboresha huduma zake kwa walipakodi, kutoa elimu ya kodi na kuwezesha biashara. 

Amesema TRA inatambua na kuthamini mchango wa Kodi wa Barrick Gold Mine wakiwa ni walipakodi wakubwa pamoja na walipakodi wengine kote nchini na kuwa milango ya taasisi hiyo ya Umma ipo wazi kwaajili ya kuwasikiliza na kutatua changamoto zinazowakabili walipakodi kote nchini.




Na Janeth Raphael - MichuziTv Bungeni Dodoma 

Mafunzo kwa vijana yanatarajiwa kwenda zaidi ya kuwapatia ujuzi, huku msisitizo ukiwekwa katika kuwaunganisha na ajira, mitaji, masoko na fursa za uzalishaji ili waweze kujiajiri na kuanzisha biashara endelevu.

Hayo yameelezwa Bungeni na Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Zainab Katimba, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Maendeleo ya Vijana, wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Zulfa Mmaka Omary, aliyetaka kujua namna Serikali inavyohakikisha programu za mafunzo na uwezeshaji kwa vijana zinazalisha ajira halisi na endelevu.

Zulfa alihoji kuhusu mkakati mahsusi wa kuhakikisha ajira na uwezeshaji wa vijana haviishii katika kuwapatia mafunzo pekee, bali vinawasaidia vijana kupata ajira, kujiajiri na kuwa na shughuli za kiuchumi zenye uwezo wa kudumu.

Akijibu, Naibu Waziri Katimba amesema mafunzo yanayotolewa kwa vijana yanaelekezwa zaidi katika mahitaji ya soko la ajira na fursa zilizopo katika shughuli za uzalishaji.

Amesema hatua hiyo inaambatana na mafunzo kwa vitendo, uanagenzi na kuwapatia vijana uzoefu wa kazi, sambamba na kuwaunganisha na mitaji, vifaa na zana za uzalishaji.

 Katimba, amesema mkakati huo unatekelezwa kupitia programu mbalimbali za uwezeshaji vijana, zikiwemo Programu ya Kukuza Ujuzi, Build for Better Tomorrow, Mining for a Brighter Tomorrow, pamoja na Programu ya Uwezeshaji Vijana Kiuchumi yenye Shilingi bilioni 200.

Programu nyingine ni Mfuko wa Maendeleo ya Vijana, mikopo ya asilimia 10 ya mapato ya ndani ya Halmashauri, pamoja na programu zinazotekelezwa na SIDO na VETA.

Aidha, amesema vijana wanaunganishwa na waajiri, taasisi za fedha, wawekezaji, masoko pamoja na fursa za ununuzi wa umma ili kuwawezesha kutumia ujuzi walioupata katika kupata ajira au kuanzisha na kukuza biashara zao.

Amesema uwezeshaji huo unaenda sambamba na ushauri wa kitaalamu, uatamiaji wa biashara, uunganishaji wa vijana katika minyororo ya thamani na masoko, pamoja na ufuatiliaji wa miradi wanayoianzisha.

Hatua hizo, kwa mujibu wa Naibu Waziri, zinalenga kuhakikisha vijana wanapata mazingira yanayowawezesha kutumia ujuzi wao kuzalisha kipato, kujenga biashara zinazodumu na hatimaye kutoa ajira kwa vijana wengine.

Amesema utekelezaji wa mikakati hiyo unafanyika kwa kushirikiana na sekta binafsi pamoja na wadau wengine wa maendeleo, kwa lengo la kujenga mfumo unaomsaidia kijana kuanzia hatua ya kupata mafunzo hadi kufikia ajira, kujiajiri au kukuza biashara yenye tija.








Na Janeth Raphael - MichuziTv Bungeni Dodoma


SERIKALI imesema itaendelea kuboresha utoaji wa mikopo ya asilimia 10 kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu kwa kuimarisha matumizi ya wataalamu wa mafunzo ya biashara, hatua inayolenga kuongeza ufanisi na manufaa ya mikopo hiyo kwa wajasiriamali nchini.

Kauli hiyo imetolewa na Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), anayeshughulikia Elimu, Dkt. Festo Dungange, wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Chiku Athman Issa.

Katika swali lake, Mbunge Chiku alitaka kujua iwapo Serikali inaona kuwa sababu kubwa ya mikopo ya asilimia 10 kutokuwa na matokeo makubwa tangu kuanza kwake ni ukosefu wa wataalamu wa kutoa mafunzo ya biashara kwa wanufaika.

Akijibu, Dkt. Dungange amesema Serikali inaendelea kutoa mikopo hiyo kwa mujibu wa Sheria ya Fedha za Serikali za Mitaa, Sura ya 290, pamoja na Kanuni zake za mwaka 2024, ambazo zinaweka utaratibu wa ukopaji, urejeshaji na usimamizi wa mikopo hiyo.

Amesema lengo la mikopo hiyo ni kuwawezesha wanawake, vijana na watu wenye ulemavu kupata mitaji midogo na ya kati isiyo na riba kupitia mapato ya ndani ya halmashauri, ili kuwawezesha kuendesha shughuli za ujasiriamali na kurejesha mikopo kwa ajili ya kuwanufaisha wajasiriamali wengine.

Dkt. Dungange amesema katika kipindi cha mwaka wa fedha 2024/25 hadi 2025/26, jumla ya vikundi 33,594 vya wajasiriamali vilinufaika na mikopo hiyo.

Amefafanua kuwa kati ya vikundi hivyo, 18,539 vilikuwa vya wanawake, 11,758 vya vijana na 3,247 vya watu wenye ulemavu, huku jumla ya Sh bilioni 357.20 zikitolewa kwa vikundi hivyo.

Dkt. Dungange, amesema kati ya fedha hizo, Sh bilioni 143.43 zilikuwa zimefikia muda wa marejesho, ambapo Sh bilioni 130.04, sawa na asilimia 91, zilikuwa tayari zimerejeshwa.

Aidha, amesema Serikali tayari imeweka mwongozo unaowataka wataalamu wa fedha, maendeleo ya jamii na wataalamu wengine waliopo katika halmashauri kushiriki katika kuwaelimisha na kuwasimamia wajasiriamali wanaoomba mikopo hiyo.

Amesema mwongozo huo pia umeweka utaratibu wa kutoa mafunzo ya masuala ya fedha na ujasiriamali kwa vikundi vinavyoomba mikopo, hatua inayolenga kuwajengea uwezo wa kutumia vizuri fedha wanazokopa na kuongeza uwezekano wa mafanikio katika shughuli zao.

“Serikali itaendelea kuboresha utoaji wa mikopo ya asilimia 10 kwa wajasiriamali kwa kuwatumia wataalamu wa mafunzo ya biashara ili kuongeza ufanisi wa mikopo hiyo,” alisema Dkt. Dungange.


Na Janeth Raphael -MichuziTv


SERIKALI kupitia Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) imeendelea kuweka mkazo katika utekelezaji wa miradi ya umeme inayolenga kuhakikisha wawekezaji katika sekta mbalimbali, ikiwemo madini, viwanda, kilimo cha kisasa na ufugaji, wanapata nishati ya uhakika kwa ajili ya kuongeza uzalishaji na kuchochea ukuaji wa uchumi.


Kauli hiyo imetolewa na Naibu Waziri wa Nishati, Salome Makamba, wakati wa hafla ya utiaji saini mkataba wa utekelezaji wa mradi wa kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 220 pamoja na kituo cha kupokea na kupoza umeme cha kilovoti 220/33 kwa ajili ya Geita Gold Mining (GGM), iliyofanyika jijini Dodoma.

Makamba amesema Serikali inalenga kufanya upatikanaji wa nishati ya uhakika kuwa miongoni mwa vivutio vikubwa vya uwekezaji nchini, kwa kuhakikisha miundombinu ya umeme inaendana na mahitaji ya uchumi na kasi ya uwekezaji.

Amesema Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan itaendelea kuwekeza katika miundombinu ya nishati ili umeme uwe kichocheo cha uzalishaji na kivutio kwa wawekezaji zaidi kuja nchini.

“Mwekezaji anapokuja Tanzania, nishati iwe kichocheo na kivutio kikubwa cha uwekezaji na uzalishaji wake,” amesema Makamba.

Amesema Serikali pia imechukua hatua za kuimarisha uwezo wa TANESCO kifedha na kiutendaji ili shirika hilo liweze kuendelea kutekeleza miradi mikubwa ya nishati. Kwa mujibu wa Makamba, Wizara ya Fedha imeidhinisha TANESCO kukopa Sh bilioni 229.3 kutoka benki za ndani kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya kimkakati yenye lengo la kuongeza mapato na kujenga uwezo wa shirika kuendelea kuwekeza.

Amesema uwekezaji huo unalenga kuhakikisha miradi ya umeme inaleta manufaa kwa pande zote, ambapo Serikali inawekeza katika miundombinu, mwekezaji anaongeza uzalishaji, TANESCO inaongeza mapato na Taifa linapata manufaa ya kiuchumi.

Makamba amesema mradi wa GGM ni mfano wa utekelezaji wa falsafa hiyo, kwa kuwa Serikali inawekeza katika miundombinu ya umeme huku mwekezaji akitarajiwa kuongeza uzalishaji, jambo litakalosaidia kuongeza mapato ya TANESCO na Serikali pamoja na kuchochea shughuli nyingine za kiuchumi.

Amesema uwekezaji katika nishati hauhusiani tu na kuwasha taa au kuendesha mashine, bali una nafasi kubwa katika kuongeza uzalishaji, kupunguza gharama za uzalishaji, kuongeza ajira, mapato ya Serikali, thamani ya rasilimali za nchi na kuvutia wawekezaji wengine.

“Tunapozungumzia uwekezaji katika nishati, tunazungumzia zaidi ya kuwasha taa au kuendesha mashine. Tunazungumzia kuongeza uzalishaji, kupunguza gharama za uzalishaji, kuongeza ajira, kuongeza mapato ya Serikali, kuongeza thamani ya rasilimali zetu na kuvutia wawekezaji wengine kuja kuwekeza nchini,” amesema.

Makamba amesema kila njia ya umeme inayojengwa, kila kituo kinachokamilishwa na kila mwekezaji anayeunganishwa kwenye Gridi ya Taifa ni sehemu ya kujenga uchumi imara, endelevu na wenye ushindani.

Amesema Wizara ya Nishati itaendelea kusimamia utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050 inayotambua nishati kuwa miongoni mwa vichocheo muhimu vya ukuaji wa uchumi na maendeleo ya nchi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Geita, Hashim Komba, ameishukuru Serikali chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa inayoendelea katika kuimarisha sekta ya nishati, akisema nishati ni eneo muhimu linalochochea maendeleo ya sekta nyingine za uzalishaji.

Komba amesema mkoani Geita kazi ya kusambaza umeme inaendelea, huku akipongeza TANESCO kwa namna inavyoendelea kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi na kugusa moja kwa moja sekta ya madini ambayo ni miongoni mwa sekta muhimu katika mkoa huo.

Amesema ongezeko la shughuli za utafiti wa madini limechochea kuongezeka kwa maeneo ya uchimbaji, hali inayosababisha mahitaji makubwa ya nishati ya uhakika kwa wachimbaji wakubwa, wa kati na wadogo.

Komba amesema mradi wa kupeleka umeme GGM haupaswi kuangaliwa kwa upande wa kusaidia mgodi pekee, bali pia kwa namna unavyoweza kuchochea uwekezaji na kuongeza mapato ya Serikali, pamoja na kuwezesha wachimbaji wadogo kupata umeme wa kutosha katika maeneo yao ya shughuli.

Amesema mkoa huo utaendelea kushirikiana na TANESCO kutoa elimu kwa wachimbaji wadogo kuhusu namna wanavyoweza kutumia fursa ya umeme katika maeneo yao ya uchimbaji, hususan kupitia Maonesho ya Teknolojia ya Madini yanayofanyika kila mwaka mkoani Geita.

Kwa mwaka huu, amesema Geita inatarajia kufanya maonesho hayo kwa mara ya tisa, huku akiahidi kuwa Serikali ya Mkoa itashirikiana na TANESCO kuhakikisha wachimbaji wadogo wanaelewa vizuri fursa zinazotokana na upatikanaji wa umeme katika maeneo yao.

Komba pia amesema Serikali ya Mkoa wa Geita imejipanga kushirikiana na mkandarasi wa mradi huo kuhakikisha utekelezaji wake unakwenda kwa wakati na kwamba changamoto zozote zinazoweza kuchelewesha mradi zitashughulikiwa kwa haraka.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Lazaro Twange, amesema uwekezaji nchini unaendelea kukua, hususan katika sekta ya madini ambayo inahitaji nishati ya uhakika kutokana na matumizi ya teknolojia na mashine za kisasa.

Twange amesema upatikanaji wa umeme wa uhakika utawawezesha wachimbaji wakubwa, wa kati na wadogo kuongeza ufanisi wa shughuli zao, kutumia teknolojia za kisasa na kuongeza uzalishaji.

Amesema TANESCO itaendelea kutekeleza miradi ya umeme kwa kuzingatia mahitaji ya wawekezaji na sekta mbalimbali za uzalishaji, ili kuhakikisha nishati inakuwa kichocheo cha shughuli za kiuchumi nchini.

Mradi wa kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 220 pamoja na kituo cha kupokea na kupoza umeme cha kilovoti 220/33 kwa ajili ya GGM unatarajiwa kukamilika ndani ya miezi 18 iliyopangwa.

Serikali imeeleza kuwa uwekezaji katika miundombinu ya umeme ni sehemu muhimu ya kuongeza uzalishaji, mapato ya TANESCO, ajira na uwekezaji, huku ukichangia kwa ujumla katika ukuaji na maendeleo ya uchumi wa Taifa.











WASUSI mbalimbali nchini wameipongeza Kampuni ya Darling Hair kwa kuwawezesha kiuchumi na kuwakwamua kutoka kwenye umaskini kupitia programu yake maalumu inayofahamika kama Loyalty.

Pongezi hizo zilitolewa katika hafla maalumu iliyofanyika Sinza, Jijini Dar es Salaam na kuwakusanya mamia ya wasusi katika hafla maalumu ya kupongezana na kutoa zawadi mbalimbali iliyoandaliwa na Darling Hair na kuhudhuriwa na uongozi wa juu kabisa wa kampuni hiyo.

“Kupitia program hii Darling Hair imetusaidia sana sisi kama wasusi na wenye masaluni kwani sasa hivi hatununui vifaa hasa viti. Tunakusanya lebo za bidhaa mbalimbali za Darling Hair na kujikusanyia pointi mbalimbali zinazotuwezesha kushinda zawadi mbalimbali,” alisema Veronica Millinga, mmoja wa wasusi aliyehudhuria hafla hiyo.

Alitoa wito kwa wasusi ambao hawajajiunga na program hiyo kuchangamkia fursa hiyo kwani faida zake ni nyingi ikiwemo baadhi ya wasusi wadogo kufungua saluni zao wenyewe.

Naye Ramadhani Kataya ambaye ni msusi na mmiliki wa saluni, alisema kupitia programu hii Darling Hair imejiweka karibu sana na wateja wake na inafuatilia hatua kwa hatua ili kuhakikisha wanapata huduma bora.

“Hawa Darling ni wabunifu sana hata mteja akija na hitaji fulani kwa haraka tu unafahamu kuwa Darling Hair wana suluhisho na ukiwapigia wanakuhudumia haraka,” alisema.

Rukia Adam, ambaye pia ni msusi, alisema program hiyo ya Loyalty imewasaidia wasusi wengi wadogo na kuwafanya wajiamini zaidi kwa kuwapa mitaji ya vifaa mbalimbali vya saluni.

“Kwa kweli wametuwezesha sana na tunaomba programu hii iwe ya kudumu ili wengi zaidi wafadike na pia itunyanyue kutoka hatua moja kwenda hatua nyingine,” alisema.

Meneja Saluni wa Darling Hair, Joyce Mwijage, alisema, awamu ya kwanza ya programu hiyo ilipata mafanikio makubwa ambapo idadi ya wasusi iliongezeka kutoka 5000 hadi 15,000.

Alisema hafla hii iliyowakusanya wasusi kutoka Tegeta, Wazo, Makonde, Boko, Bunju, Tanki Bovu, Mivumoni, Kunduchi na Kawe ni ya pili tangu kampuni hiyo izindue awamu ya pili ya program hiyo iliyoanza 2024. “Baada ya Dar es Salaam tutaenda mikoa mbalimbali ili tuwafikie wasusi nchi nzima,” alisema.

Alisema washiriki walikusanya lebo za bidhaa za Darling Hair na kujizolea pointi kadhaa ambazo ziliwawezesha kujipatia zawadi mbalimbali.

“Lengo la program hii ya Loyalty ni kuwazawadia wasusi wadodo wadogo ili waweze kujiendeleza na hatimaye kufungua saluni zao wenyewe kutokana na vifaa vya saluni wanavyojishindia kwa kukusanya lebo za bidhaa zetu na kujizolea pointi kwa kila lebo.”Alisema.

Aliongeza kuwa baada ya Dar es Salaam.watahamia katika mikoa mingine ambapo amewataka wasusi hao kujipanga kwa kampeni hiyo ambayo kwa mujibu wa meneja huyo, ni ya kudumu.

Kulikuwa na zawadi, michezo mbalimbali, mziki uliopambwa na wasanii mbalimbali akiwemo msanii maarufu, Click Master ambaye hakuwaangusha mashabiki wake kwa kuimba nao nyimbo kama Watajua na Sherehe.

MCHEZO wa kasino Wild White Whale umeendelea kuvutia macho ya wapenzi wa burudani za kasino, na sasa Meridianbet imeongeza msisimko mwingine kupitia promosheni inayompa kila mchezaji nafasi ya kupata mizunguko 50 ya bure. Kupitia ofa hii, wabashiri wanaweza kufungua zawadi hiyo kila wanapokamilisha mizunguko 100 kwenye mchezo huo. Ni fursa inayoongeza ladha ya mchezo huku kila mzunguko ukiwa na nafasi ya matokeo mapya.

Kinachofanya promosheni hii iwe na mvuto zaidi ni kwamba mizunguko 50 ya bure hutolewa bila kujali matokeo ya mizunguko 100 ya awali. Hivyo, kama umefanikiwa kupata ushindi au haujapata matokeo uliyotarajia, bado unapata zawadi yako baada ya kutimiza idadi inayotakiwa. Kwa lugha rahisi, safari yako ya mizunguko 100 haimalizii hapo, bali inafungua mlango wa mizunguko mingine 50 ya ziada ambayo huongezwa moja kwa moja kwenye akaunti yako.

Vilevile, meridianbet wana michezo mingi ya kasino mtandaoni na mechi za kimataifa za kubashiri zenye ushindani mkubwa wa odds. Jiunge leo kwa kutembelea tovuti ya meridianbet au piga *149*10# kisha uanze safari yako ya ushindi.

Ili kuingia kwenye mchezo huu, mchezaji anatakiwa kuwa na akaunti ya Meridianbet na kucheza Wild White Whale kwa kutumia pesa halisi. Baada ya kukamilisha mizunguko 100, mfumo huongeza mizunguko 50 ya bure kwenye akaunti yako. Hata hivyo, ofa hii inahesabiwa kwa mteja mmoja kwa kila akaunti, hivyo kila mshiriki anapaswa kuhakikisha anatumia akaunti yake halali na kufuata masharti yaliyowekwa kwenye promosheni.

Habari nyingine njema ni kwamba mizunguko hiyo ya bure haina masharti ya kucheza tena, hivyo ushindi unaopatikana kupitia mizunguko hiyo unaweza kufurahiwa kwa uhuru kulingana na masharti ya mchezo. Meridianbet pia imeweka wazi kuwa inaweza kubadilisha au kusitisha promosheni hiyo wakati wowote bila kutoa taarifa ya awali. Kwa hiyo, wapenzi wa kasino wanaovutiwa na ofa hii wanapaswa kufuatilia masharti yake na kutumia fursa hiyo ikiwa bado inapatikana.

Kwa ujumla, Wild White Whale sasa ina sababu nyingine ya kuwavuta wachezaji wanaotafuta burudani yenye msisimko zaidi, huku mizunguko 50 ya bure ikiongeza nafasi ya kuendelea na mchezo baada ya kutimiza mizunguko 100. Kama unataka kuingia kwenye safari hii ya baharini yenye msisimko, tembelea tovuti ya Meridianbet au tumia application ya Meridianbet, chagua Wild White Whale na uanze mchezo.

Ipswich Town wanawakaribisha Liverpool katika uwanja wao wa Portman Road, Ijumaa ya leo majira ya saa 22:00 usiku, mchezo huu ni mzunguko wa tatu wa msimu wa 2026/27 wa Ligi Kuu ya Uingereza, na mechi hii inatarajiwa kuwa na mvuto mkubwa kutokana na hali za timu hizi mbili kutokana na michezo yao ya awali msimu huu.

Ipswich Town wamerudi Ligi Kuu baada ya kutwaa nafasi ya pili katika Championship msimu uliopita. Wameanza msimu vizuri kwa ushindi wa 2-1 dhidi ya Sunderland nyumbani, lakini walipata pigo kubwa la kufungwa mabao 5-2 na Manchester United huko Old Trafford.

Hata hivyo Matokeo hayo yanaonyesha kuwa Ipswich wana nguvu mbele lakini wana upungufu mkubwa katika ulinzi, wakiwa wamefunga mabao manne na kufungwa sita katika mechi mbili za kwanza.

Kwa upande wa Liverpool, msimu wao umeanza kwa uchovu kidogo timu hiyo imepata sare mbili mfululizo katika mechi zao za awali, ikionyesha usawa wa mabao manne kufunga na manne kufungwa.

Hata hivyo, takwimu za uchezaji binafsi wa wachezaji zinaonyesha Liverpool bado wana ubora wa hali ya juu kwenye uwanja, hata kama matokeo ya mechi za awali hayajaonyesha hilo bado.

Meridianbet inasema kuna michezo kama Keno, Aviator, Poker, Roulette, Wild Icy Fruits, Super Heli. Ingia katika kasino ya mtandaoni ya Meridianbet na ujiokotee mkwanja mapema. Jiunge sasa au Tembelea tovuti ya meridianbet.co.tz au piga *149*10# kisha uanze safari yako ya ushindi.

Kihistoria, Liverpool wana rekodi kubwa dhidi ya Ipswich, wakiwa wameshinda mechi 39 kati ya 74 walizocheza dhidi yao, huku Ipswich wakishinda mara 14 tu na sare 21. Mchezo wao wa mwisho ulimalizika kwa ushindi mkubwa wa Liverpool wa mabao 4-1, jambo linaloonyesha wazi ubora wa Liverpool katika historia ya ana kwa ana.

Wachezaji wa kufuatiliwa ni pamoja na Abdul Fatawu na Julio Enciso kwa upande wa Ipswich, ambao wamekuwa wajenga mashambulizi ya ubunifu eneo la mbele, huku Liverpool wakitegemea nguvu zao za kawaida za mashambulizi , ili kurejesha mwendo wao baada ya sare mbili za awali.

Kutokana na umuhimu wa mechi hii kwa Ipswich, ambao wanahitaji pointi za haraka kuimarisha msimamo wao wa msimu huu wa kwanza tangu kurejea ligi kuu.

Na Said Mwishehe,Michuzi TV

KAMPUNI ya Jubilee Life Insurance Tanzania imezindua bidhaa tatu mpya za bima ya maisha zinazolenga kuwasaidia Watanzania katika uwekaji akiba, maandalizi ya elimu, ulinzi wa maisha na mahitaji mengine ya kifedha ya baadaye.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa bima hizo jijini Dar es Salaam Ofisa Mtendaji Mkuu wa Jubilee Life Insurance Tanzania, Helena Mzena, amezitaja bima walizozindua ni Fanaka Plus, Smart Education Insurance Plan na Akiba Flex.

“Kwa miaka zaidi ya 10 tumekua tukitoa suluhisho la bima za maisha ambazo kimsingi zinampa mteja wetu nafasi ya kutimiza malengo yake aliyojiwekea kama vile kusomesha Watoto Pamoja na kukuza biashara zao huku wakiwa na ulinzi wa maisha yao.

“Kwa kujali na kuzingatia matakwa ya Watanzania wote, kwa Pamoja kama taasisi tumeona ni vyema kuendelea kuboresha bidhaa zetu hizi ili kuwa na manufaa zaidi kwa wateja wetu,”amesema Mzena 

Akieleza zaidi amesema bima yao kwa ajili ya uwekezaji ambayo ilikua ikijulikana kama FANAKA LIFE PLAN, sasa inaitwa FANAKA PLUS ikiwa na maboresho zaidi yanayomhakikishia mteja wetu ongezeko la fedha zake, ulinzi wa maisha yake Pamoja na amani ya moyo akijua hakuna janga au changamoto itayozuia utimiaji wa ndoto zake, yote haya na mengine mengi sasa yanapatikana ndani ya FANAKA PLUS.

Pia amesema wameboresha bima yetu ya Maisha ya Akiba flex ambayo yenyewe inamruhusu mteja wao kuchangia kwa ajili ya mkataba wake wa bima ya maisha huku ikimpa uhuru wa machangio yake pale anapohitaji.

“Hatukuwaacha nyuma wazazi ambao wanajali elimu ya Watoto wao, na rasmi tunatambulisha kwenu SMART EDUCATION, hii ni bima ya maisha kwa ajili ya maandalizi ya ada ya mtoto, hapa mteja wetu anaweka akiba yake ili kuhakikisha ndoto za kielimu za Watoto wake zinatimia…

“Huku akiwa na ulinzi wa maisha yake na uhakika wa kwamba sisi Jubilee Life Insurance tutawajibika kutimiza ndoto hizo hata bila uwepo wa huyu mzazi,”amesema.

Ameongeza bima zote hizo ni uthibitisho wa kwamba sisi kama taasisi tunajali na kuthamini ndoto za wateja wetu na kuhakikisha ndoto hizo zinafikiwa bila stress zozote.”Sisi tunasema, Bima ya Maisha ni ya kila mmoja.”

Kwa upande wake mwakilishi wa Kamishna kutoka TIRA, Alex Rocky amesema ubora wa bidhaa za bima haupaswi kupimwa kwa idadi ya watu waliojiunga pekee, bali pia kwa kiwango ambacho bidhaa hizo zinawawezesha wananchi kuelewa na kutumia huduma za bima kwa ufanisi.

“Uelewa hujenga imani, na imani huongeza matumizi endelevu ya bima,” amesema.

Amesema Tanzania inaingia katika hatua muhimu ya kujenga familia zenye uwezo wa kustahimili misukosuko ya kifedha na taifa lenye uimara wa kifedha, huku bima ya maisha ikiwa na nafasi muhimu katika kulinda wananchi na kusaidia mipango yao ya muda mrefu.

Amesema matumizi ya lugha ya Kiswahili katika bidhaa hizo ni hatua muhimu katika kuongeza uelewa na ujumuishi wa huduma za bima nchini.

“Matumizi ya lugha inayoeleweka katika kutoa taarifa na elimu kuhusu bima huwawezesha wananchi kuelewa kwa usahihi faida, masharti na wajibu wao kabla na baada ya kujiunga na bima,” amesema.

Pia amesema bima ya maisha ni nyenzo muhimu katika kujenga usalama wa kifedha na uwezo wa kustahimili changamoto kwa mtu binafsi, familia na taifa kwa ujumla



Top News