Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali itaendelea kuthamini na kuimarisha ushirikiano na sekta binafsi katika sekta ya elimu kutokana na mchango wake mkubwa kwenye kuongeza ubora wa elimu na kuandaa rasilimali watu yenye maarifa, ujuzi na maadili yanayohitajika katika maendeleo ya Taifa.

Dkt. Mwigulu amesema hayo alipokuwa Mgeni Rasmi katika Mahafali ya 11 ya wahitimu wa Kidato cha Nne (Year 11–IGCSE) wa mwaka wa masomo 2025/2026 ya Shule ya Kimataifa ya Feza yaliyofanyika Salasala, Dar es Salaam, leo Ijumaa, Juni 12, 2026.

"Nimekuja leo kwa kuwa Serikali inayoongozwa na Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, inatambua ubia huu muhimu ambao shule yenu imekuwa ikifanya katika sekta ya elimu. Hatuwezi kuyataja mafanikio katika sekta ya elimu bila kutaja mchango wa shule za sekta binafsi, na kwa umuhususi shule za Feza," amesema Dkt. Mwigulu.

Amesema Taasisi ya Feza ni miongoni mwa taasisi zilizochangia kwa kiasi kikubwa mageuzi ya elimu nchini kwa kuweka viwango vya juu vya ubora wa elimu vinavyotambulika ndani na nje ya Tanzania.

"Hatungeweza kutaja mabadiliko na mageuzi makubwa yaliyofanyika katika sekta ya elimu bila kutaja mchango wa shule za Feza. Mmekuwa chachu ya mageuzi makubwa yaliyofanyika katika sekta ya elimu," amesema.

Aidha, Waziri Mkuu ameipongeza Taasisi ya Feza kwa kuendelea kuvutia wanafunzi kutoka mataifa mbalimbali duniani, hatua inayoonesha kiwango cha ubora wa elimu inayotolewa na taasisi hiyo.

"Sina shaka nyote mtakubaliana nami kuwa viwango vya ubora wa shule hizi vimekuwa chachu ya kuvutia wanafunzi kutoka mataifa mbalimbali ikiwemo India, Uturuki, China, Falme za Kiarabu, Lebanon, Somalia, Marekani na nchi nyingine," amesema.

Waziri Mkuu amesema Serikali inaendelea kutekeleza mageuzi mbalimbali katika sekta ya elimu ili kuhakikisha mfumo wa elimu unaendana na mahitaji ya sasa ya dunia pamoja na maendeleo ya sayansi na teknolojia.

Amesema mojawapo ya hatua hizo ni utekelezaji wa Sera ya Elimu na Mafunzo ya Mwaka 2014, Toleo la 2023, inayolenga kuimarisha upatikanaji wa elimu bora na kufanya elimu ya lazima kuwa ya miaka 10.

"Tumeyafanya mageuzi haya kwa kuzingatia mabadiliko makubwa yanayotokea duniani na kwa lengo la kuwaandaa vijana wa Kitanzania kukabiliana na changamoto na fursa za dunia ya sasa," amesema.

Sambamba na hilo, Dkt. Mwigulu ameipongeza Taasisi ya Feza kwa mchango wake katika utekelezaji wa miradi ya uwajibikaji kwa jamii ikiwemo kusaidia wanafunzi wenye uhitaji, kuboresha miundombinu ya shule za umma na kuchimba visima vya maji katika maeneo mbalimbali nchini.

Akizungumzia nafasi ya elimu katika maendeleo ya Taifa, Waziri Mkuu amesema uwekezaji katika rasilimali watu ndiyo msingi wa maendeleo endelevu ya nchi yoyote duniani.

"Hakuna nchi yoyote iliyowahi kuendelea bila kuwekeza katika rasilimali watu ya kiwango cha juu. Hizi rasilimali nyingine zinaweza zisiwepo, lakini ukiwa na watu wenye maarifa, ujuzi na maadili unaweza kujenga Taifa lenye maendeleo makubwa," amesema.

Aidha, amewataka wahitimu kuendelea kuwa na nidhamu, kutumia maarifa waliyojifunza kwa manufaa ya jamii na Taifa, pamoja na kutumia mitandao ya kijamii kwa tija.

"Mkawe mabalozi wazuri wa mafunzo mliyoyapata hapa. Mafanikio ya kweli hayatapimwa kwa matokeo ya mitihani pekee, bali kwa aina ya watu mtakaokuwa baada ya hapa," amesema.





Na Chalila Kibuda, Michuzi TV

Chama cha Wafanyakazi wa Ukusanyaji wa Mapato Tanzania (TAREWU) kimesaini hati ya makubaliano ya ushirikiano wa miaka mitano na kampuni ya BodyMind Insight (BMI) kwa lengo la kuimarisha afya ya akili, ustawi wa kisaikolojia na maendeleo ya wafanyakazi nchini.

Hafla ya utiaji saini wa makubaliano hayo imefanyika katika ofisi za BMI jijini Dar es Salaam, ambapo viongozi wa pande zote mbili walisisitiza umuhimu wa kuweka afya ya akili katika nafasi ya juu ndani ya mazingira ya kazi.

Akizungumza mara baada ya kusaini makubaliano hayo, Katibu Mkuu wa TAREWU, Dkt. Michael Marere, alisema chama hicho kimeamua kuweka kipaumbele katika kulinda afya ya akili na ustawi wa wanachama wake ili kuongeza ufanisi kazini na kuboresha maisha yao kwa ujumla.

Alisema kupitia ushirikiano huo, wanachama wa TAREWU watapata elimu kuhusu afya ya akili, ustawi wa kisaikolojia na mbinu za kukabiliana na changamoto mbalimbali zinazoweza kuathiri utendaji wao wa kazi.

“Makubaliano haya yatadumu kwa kipindi cha miaka mitano na yanaweza kuongezwa baada ya muda huo kuisha kulingana na mafanikio yatakayopatikana,” alisema Dkt. Marere.

Aliongeza kuwa afya ya akili imekuwa suala muhimu katika mazingira ya kazi ya kisasa na inahitaji kupewa uzito sawa na afya ya mwili kutokana na mchango wake katika kuongeza tija na ubunifu kazini.

“Wafanyakazi wenye afya bora ya akili huongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao na kuchangia maendeleo ya taasisi pamoja na taifa kwa ujumla. Katika mazingira ya kazi yanayobadilika kwa kasi, ni muhimu kuwawezesha wafanyakazi kujenga ustahimilivu wa kukabiliana na changamoto za maisha na kazi,” alisema.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa BMI, John Ambrose, alisema afya ya akili ndiyo msingi wa mafanikio ya mtu binafsi na taasisi, akisisitiza umuhimu wa kujenga mazingira salama yanayozingatia ustawi wa wafanyakazi.

Ambrose alisema changamoto za afya ya akili zinaendelea kuongezeka duniani, huku ripoti ya Afya ya Akili Mahali pa Kazi ya mwaka 2026 ikionyesha kuwa asilimia 61 ya wafanyakazi wameongeza matumizi ya likizo zinazohusiana na afya ya akili mwaka huu.

Aliongeza kuwa asilimia 36 ya wafanyakazi duniani wanakabiliwa na matatizo ya usingizi, hali inayotajwa kuwa miongoni mwa changamoto kubwa za afya ya akili zinazowaathiri wafanyakazi wengi huku viongozi wengi wa taasisi wakikosa uelewa wa kutosha kuhusu tatizo hilo.

Aidha, alisema mzigo wa mikopo kutoka taasisi za kifedha umeendelea kuwa chanzo kingine cha msongo wa mawazo na changamoto za afya ya akili kwa wafanyakazi na makundi mbalimbali ya jamii.

Ambrose alisema ushirikiano kati ya BMI na TAREWU utasaidia kuongeza uelewa wa masuala ya afya ya akili na kuweka mifumo bora ya kusaidia wafanyakazi kuwa na ustawi unaochochea maendeleo ya mtu mmoja mmoja na taasisi kwa ujumla.

Mkuugenzi wa BodyMind Insight Dkt.John Ambrose akizungumza namna watavyotoa huduma kwa wanachama wa TAREWU kuhusiana Afya ya Akili na Saikolojia katika maeneo ya kazi

Katibu Mkuu wa Chama cha Wafanyakazi wa Ukusanyaji Mapato Tanzania (TAREWU) Dkt.Michael Marere akizungumza na waandishi wa habari kuhusiana TAREWU kuingia makubaliano na BodyMind Insight (BMI) kwa ajili ya wanachama wao kupata elimu ya afya ya akili na Saikolojia .
Hati zikioneshwa mara baada ya kusaini makubaliano baina ya Taasisi hizo mbili.
Katibu Mkuu wa Chama cha Wafanyakazi wa Ukusanyaji Mapato Tanzania (TAREWU) Dkt.Michael Marere na Mkurugenzi wa BodyMind Insight (BMI) Dkt.John Ambrose wakisaini hati za makubaliano katika hafla iliyofanyika Ofisi za BMI jijini Dar es Salaam.

-Ni inayozungumzia usafirishaji dawa za kulevya katika vyombo vya usafiri


Na Said Mwishehe,Michuzi TV

FILAMU iliyopewa jina la Kifurushi ambayo inalenga kuendelea kutoa elimu kwa jamii kuhusu mapambano dhidi ya dawa za kulevya imezinduliwa rasmi na itakuwa inaoneshwa katika mabasi yote yanayosafiri mikoa mbalimbali nchini.

Akizungumza leo Juni 12,2026 katika Kituo Kikuu cha Mabasi cha Magufuli kilichopo Mbezi jijini Dar es Salaam Kamishina Jenerali wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya Aretas Lyimo amesema mamlaka hiyo ilifanya majadiliano na LATRA na Bodi ya Filamu Tanzania na kuona umuhimu wa kuandaa filamu itakayooneshwa katika mabasi yote yanayosafiri mikoa kmbalimbali nchini.

Amesema hatua hiyo ni kama moja ya njia ya kutoa elimu kwa jamii ili kuzuia athari zinazoweza kusababishwa na usafirishaji wa dawa za kulevya.Filamu hiyo fupi imeandaliwa kuonesha uhalisia wa namna ambavyo mtu anaweza kuingia kwenye mtego wa kuwa sehemu ya wahalifu, kusafirisha dawa za kulevya kwa kubeba.

“Au kusafirisha mzigo auvifurushi asivyovifahamu pamoja na kutambua madhara ya kijamii na kiuchumi yanayoweza kujitokeza kutokana na kitendo hicho.Ni kwa msingi huo tumekuja na ‘’Kaulimbiu isemayo, Usafiri Salama bila dawa za kulevya.

Aidha amesema filamu hiyo inalenga kuongeza uelewa kwa madereva,makondakta, wahudumu wa mabasi, wasafirishaji wa mizigo, abiria na wananchi kwa ujumla kuhusu wajibu wao katika vita dhidi ya dawa za kulevya kwa kutoa taarifa za vitendo vinavyohusiana na usafirishaji wa dawa za kulevya.

Akieleza zaidi kuhusu sababu za kuja na filamu hiyo amesema dawa za kulevya ni tishio kubwa kwa afya za wananchi, ustawi wa familia, usalama wa jamii na maendeleo ya taifa letu na kwamba madhara ya dawa za kulevya yanachangia kuongezeka kwa changamoto za kiafya, uhalifu, kuzorota kwa familia, uvunjifu wa amani, pamoja na kudhoofika kwa nguvu kazi ya taifa, hususan vijana na hatimaye huathiri maeneo muhimu ya kiuchumi.

“Kutokana na athari hizo, Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi thabiti wa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kushirikiana na wadau mbalimbali imeendelea kuchukua hatua madhubuti za kudhibiti biashara na matumizi ya dawa za kulevya.”

Amefafanu hatua hizo zinajumuisha operesheni za ukamataji, tiba kwa waathirika wa dawa za kulevya, uchunguzi wa makosa ya dawa za kulevya pamoja na utoaji wa elimu kwa umma ili kujenga uelewa na ushiriki wa wananchi katika mapambano haya.

Ameongeza pia kwa siku za hivi karibuni, Mamlaka imeendelea kubaini mbinu mbalimbali zinazotumiwa na wahalifu kusafirisha dawa za kulevya ikiwemo kupitia vyombo vya usafiri wa umma.

“Mara nyingi dawa hizo hufichwa kwenye mizigo na vifurushi vinavyoonekana kuwa vya kawaida.Baadhi ya wananchi, abiria na hata wahudumu wa ndani ya vyombo vya usafiri wamejikuta wakihusishwa na makosa ya dawa za kulevya baada ya kubainika kubeba mizigo wasiyoifahamu.

“Ninitumie fursa hii kuwaomba wamiliki wa mabasi, makampuni ya usafirishaji na wadau wote wa sekta ya usafiri kuipokea na kuipa kipaumbele filamu hii kwa kuhakikisha inaoneshwa katika vyombo vyao vya usafiri.

“Ushirikiano wenu utasaidia kuwafikia kwa haraka wananchi wengi kila siku na kufanya kila safari kuwa fursa ya kutoa elimu na kuimarisha usalama wa jamii dhidi ya tatizo la dawa za

kulevya.Tumechagua kuzindua filamu hii hapa Kituo Kikuu cha Mabasi cha Magufuli kwa sababu ni moja ya kituo kikubwa zaidi nchini kinachohudumia maelfu ya wasafiri kila siku.”

Aidha ametumia nafasi hiyo kutoa ujumbe kwa jamii ya Watanzania kwamba “Usikubali kubeba mzigo, kifurushi au bidhaa yoyote usiyoifahamu. Hakikisha unatambua unachobeba, kinatoka kwa nani na kinaelekea kwa nani. Kifurushi unachodhani ni cha kawaida kinaweza kubeba dawa za kulevya na kubadili maisha yako kwa matokeo hasi”.

Ameongeza kwa pamoja tunaweza kuzuia usafirishaji wa dawa za kulevya, kulinda vijana wetu, kuimarisha usalama wa jamii na kujenga Taifa lenye afya, nguvu kazi salama na maendeleo endelevu kupitia ujumbe uliopo kwenye filamu hiyo.





KUTOKA VUNJO.

KATIKA kuhakikisha kuwa wananchi wa Jimbo la Vunjo wanakabiliana na tatizo la uhaba wa ajira kwa kujiajiri wenyewe, Mbunge wa jimbo hilo Enock Koola amekuja kampeni maalum ya kuwafundisha wananchi ufugaji wa ng'ombe wa maziwa pamoja na samaki.

Mafunzo hayo yanayotarajiwa kutolewa kesho Juni 13 mwaka huu katika ukumbi wa shule ya viziwi kata ya njia panda.

Mafunzo hayo yatawasidia wananchi kujiajiri kupitia ufugaji wenye faida na kuwawezesha vijana kupata fursa ya ajira.

Hili ni mwendelezo wa juhudi za Mbunge Enock Koola ya kuhakikisha anainua uchumi wa wananchi wa jimbo hilo ambapo hapo awali alikuja na mkakati wa kufufua zao la kahawa kwa kuleta miche bora na ya kisasa kwa maeneo yanayolima zao hilo.

Katika kampeni ya miche bora ya miparachichi jumla ya vijana 60 walinufaika katika jimbo hilo, elimu ya ufugaji nyuki vijana 80 walinufaika, huku upande wa uvuvi na ufugaji ng'ombe vijana 80 watanufaika kutoka kila kata ili kwenda kutoa elimu kwa wananchi na vijana wengine.




Na Mwandishi Wetu

Baraza la Ushindani Halali Zanzibar (ZFCT) limefanya ziara ya mafunzo katika Tume ya Ushindani ya Haki (FCC) kwa lengo la kujifunza na kubadilishana uzoefu katika masuala ya ushindani wa biashara, udhibiti wa bidhaa bandia pamoja na usimamizi wa mashauri yanayohusiana na ushindani.

Ziara hiyo iliyofanyika katika ofisi za FCC Juni 10, 2026 Jijini Dar es Salaam, imeelezwa kuwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha ushirikiano kati ya taasisi hizo mbili ili kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao na kuhakikisha mazingira ya biashara yanakuwa ya haki kwa wadau wote.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, Bi. Khadija Ngasongwa alisema kuwa kubadilishana uzoefu na taasisi za ndani ya nchi ni muhimu katika kuimarisha mifumo ya usimamizi wa ushindani na kulinda maslahi ya watumiaji dhidi ya vitendo vinavyokiuka sheria za ushindani na biashara.

Alisema ujumbe wa ZFCT unapata fursa ya kujifunza namna FCC inavyotekeleza majukumu yake ya kudhibiti vitendo vya ushindani usio wa haki, kukabiliana na biashara ya bidhaa bandia pamoja na mifumo ya uchunguzi na uendeshaji wa mashauri mbalimbali yanayofikishwa mbele ya taasisi hiyo.

Kwa upande wake, ujumbe wa ZFCT ukiongozwa na Msajili wa Baraza, Bi. Fatma Yahya alieleza kuridhishwa na mafunzo na uzoefu uliopatikana katika ziara hiyo, ukibainisha kuwa utaisaidia taasisi hiyo kuimarisha utendaji wake katika kushughulikia rufaa na mashauri yanayohusiana na ushindani wa biashara Zanzibar.

ZFCT ni chombo kinachoshughulikia mashauri na rufaa zinazotokana na maamuzi ya mamlaka za ushindani, ambapo wadau wasiokubaliana na maamuzi yaliyotolewa huwasilisha kesi zao kwa ajili ya kusikilizwa na kutolewa uamuzi.

Ziara hiyo pia ilitoa nafasi kwa wataalamu kutoka pande zote mbili kujadiliana changamoto na fursa zilizopo katika usimamizi wa ushindani wa biashara, huku wakisisitiza umuhimu wa kuendelea kushirikiana katika kujenga uwezo wa kitaasisi na kuimarisha utekelezaji wa sheria zinazolinda ushindani wa haki katika soko.

DODOMA Jiji wametwaa ubingwa wa jumla wa mashindano ya UMISSETA ngazi ya mkoa 2026 baada ya kuonyesha kiwango cha juu cha ushindani na kujikusanyia alama 255 zilizowahakikishia nafasi ya kwanza.

‎Ushindi huo umechangiwa na mwendelezo mzuri wa matokeo katika michezo mbalimbali ambapo wamenyakua vikombe 10, ikiwemo mpira wa kikapu (wavulana na wasichana), mpira wa mikono (wavulana na wasichana), mpira wa wavu wavulana, soka wasichana na kizazi kipya, huku wakimaliza nafasi ya pili katika mpira wa wavu wasichana.

‎‎Akizungumzia ushindi huo, Afisa Elimu Sekondari wa Jiji la Dodoma, Mwl. Daniel Mapilya, alisema mafanikio hayo yameambatana na uwakilishi mkubwa katika timu ya mkoa, ambapo kati ya wanafunzi 120 waliochaguliwa, 45 wametoka Jiji la Dodoma, hatua inayoonesha ubora wa maandalizi kuelekea mashindano ya kitaifa yatakayofanyika Iringa.

“Mafanikio hayo ni makubwa kwa jiji letu, na tunawapongeza walimu wa michezo, wakuu wa shule, maafisa utamaduni na michezo pamoja na maafisa elimu sekondari kwa mchango wao mkubwa uliowezesha ushindi huu kupatikana” alisema Mwl. Mapilya.

‎Nae, Afisa Michezo wa Jiji la Dodoma, Peter Ititi alisema mafanikio hayo yamechangiwa na ushirikiano mzuri kutoka kwa Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma, Mkuu wa Wilaya ya Dodoma na Mbunge wa Jimbo la Mtumba ambao wamekuwa wakiwapa hamasa. Aliahidi kuwa wataendelea kufanya vizuri na kuongeza idadi ya makombe katika mashindano yajayo.

‎‎Kwa upande wake, Mchezaji wa Mpira wa Miguu wa Dodoma Jiji, Fortunata Mfaume aliyeteuliwa kuwakilisha timu katika mashindano ya kitaifa yatakayofanyika mkoani Iringa, alisema kuwa amejipanga kikamilifu kuhakikisha anatoa mchango wake kwa timu ya mkoa na kuiwezesha kufanya vizuri katika mashindano hayo.

‎Mafanikio ya Dodoma Jiji katika mashindano ya UMISETA ngazi ya mkoa 2026 yanadhihirisha maandalizi mazuri, mshikamano na ushindani wa hali ya juu. Timu hiyo sasa inaelekeza macho yake katika mashindano ya kitaifa, ikilenga kuendeleza rekodi yake ya ubabe kimichezo.







Wakulima nchini wametakiwa kutumia mbegu bora wanapopanda mazao yao ili kuongeza uzalishaji wa mazao yenye ubora wa juu yatakayowezesha kupata bei nzuri kwenye masoko ya ndani na nje ya nchi.

Wito huo umetolewa na Afisa Mtendaji Mkuu wa Soko la Bidhaa Tanzania (TMX), CPA. Godfrey Malekano, wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari kutoka mikoa ya Dar es Salaam, Dodoma, Iringa na Singida yaliyofanyika jijini Dodoma Juni 12, 2026.

CPA. Malekano alisema ubora wa mazao ndiyo msingi mkuu wa upatikanaji wa bei nzuri sokoni, akisisitiza kuwa matumizi ya mbegu bora ni hatua muhimu kwa mkulima kufikia mafanikio ya kiuchumi.

Alisema utaratibu wa wanunuzi kununua mazao moja kwa moja mashambani bila kuyapeleka kwenye mfumo rasmi wa soko umepitwa na wakati, kwani kwa sasa wakulima wana fursa ya kupata bei shindani kupitia mfumo wa TMX uliorasimishwa na Serikali.

“Unapouza mazao nje ya mfumo rasmi, si mkulima pekee anayepoteza fursa ya kupata thamani halisi ya mazao yake, bali hata Serikali inapoteza matokeo ya uwekezaji wake mkubwa katika utoaji wa pembejeo za ruzuku kwa wakulima."

Aliongeza kuwa TMX inaendelea na jitihada za kuhakikisha bidhaa zote za kilimo zinauzwa kupitia soko hilo kama ilivyo katika mataifa mengi yaliyoendelea, Kwa sasa, bidhaa 11 tayari zinauzwa kupitia mfumo huo ikiwemo madini ya Vito.

Aidha, alisema maendeleo ya teknolojia yameongeza uelewa wa wakulima kuhusu mwenendo wa bei za mazao katika soko la dunia kupitia matumizi ya simu janja, hali inayowasaidia kufanya maamuzi sahihi ya biashara.

“Leo hii mkulima anafuatilia bei za mazao akiwa kijijini kupitia simu yake, ndiyo maana wanunuzi wanaotaka kununua kwa bei ya chini hukataliwa kwa sababu wakulima wengi wanatambua thamani halisi ya mazao yao."

Kwa upande wake, Ofisa wa TMX, Justa Martine, alisema kuuza mazao kupitia Soko la Bidhaa Tanzania kuna manufaa makubwa kwa wanunuzi na wauzaji.

Alieleza kuwa mfumo huo hupunguza gharama za mnunuzi kufika eneo la mzigo, huongeza uwazi wa biashara kwa kuonyesha ubora wa bidhaa na mwenendo wa bei sokoni, na pia humpa muuzaji uhuru wa kukubali au kukataa kuuza endapo hajaridhishwa na bei inayotolewa.

TMX inaendelea kuhamasisha wakulima na wadau wa sekta ya kilimo kutumia mfumo wa soko la bidhaa ili kuongeza tija, uwazi na ushindani katika biashara ya mazao nchini.




Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa - TAKUKURU Mkoa wa Geita, imewafikisha mahakamani watumishi wa umma saba kwa tuhuma za ubadhirifu wa fedha za Serikali zaidi ya Sh milioni 78.

Akizungumza na wanahabari leo Juni 12, 2026, Mkuu wa TAKUKURU Geita amesema watumishi hao walikusanya mapato kupitia mfumo wa LGRCIS kwa kutumia mashine za POS lakini hawakuwasilisha fedha hizo katika akaunti ya Serikali.

"Uchunguzi umebaini watumishi hao walisababisha Serikali kupata hasara ya jumla ya Sh78,875,110/= kinyume na utaratibu," amesema.

Watumishi hao ni: Tatu Jeki Kijungu - Afisa Hesabu Wilaya ya Geita, Sylvanus Ngoya Michael - Mhasibu Wilaya, Ladislaus Katuma Kamhanda - Afisa Mtendaji Kata Nyamalimbe, Melina Damian Buguba - Afisa Uvuvi, Mtani Daniel Yangwe na Allen Michael Kimaro - Makusanya Mapato Manispaa, na Mashalla Charles Nkwande - Afisa Mtendaji Kata Kakubilo.

Baada ya kupata vibali kutoka Ofisi ya Taifa ya Mashtaka, mashauri 7 yamefunguliwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Geita leo kwa nambari ECO.13145/2026 hadi ECO.13153/2026.



 

Wakulima wa zao la pamba kutoka vijiji vya Mbutu, Iyogelo, Ilambakuki, Imalanguzu na Mwamakoma vilivyopo katika Wilaya ya Igunga, Mkoa wa Tabora, wamehamasika kufungua akaunti za benki na kusajili laini za simu ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya kupokea malipo ya mazao yao kwa njia ya kidijitali. Hatua hiyo inalenga kuongeza uwazi, usalama na uharaka wa malipo kwa wakulima.

Wakulima hao wamefungua akaunti kupitia Benki ya NMB pamoja na kusajili laini kupitia mtandao wa simu wa Mixx by Yas, hatua itakayowawezesha kupokea fedha zao kwa urahisi kupitia mifumo ya benki na huduma za kifedha za simu za mkononi.

Zoezi hilo limefanyika kwa kushirikiana na AMCOS za Ngw'ajojabi, Ngw'asabi na Mwamakoma AMCOS, likitekelezwa kufuatia waraka wa Mrajis wa Vyama vya Ushirika unaoelekeza malipo ya wakulima wa pamba kufanyika kupitia akaunti za benki na huduma za fedha kwa njia ya simu badala ya kutegemea fedha taslimu. Lengo ni kuhakikisha wakulima wanapata malipo yao kwa wakati, kwa uwazi na kwa usalama zaidi.

Mwitikio wa wakulima umeendelea kuongezeka siku hadi siku kufuatia juhudi za uhamasishaji zinazoendelea kufanyika katika maeneo mbalimbali. Hadi kufikia Juni 10, 2026, jumla ya wakulima 506 wamejitokeza na kufungua akaunti pamoja na kujiunga na huduma za kifedha za simu, hatua inayoonesha uelewa na utayari mkubwa wa wakulima kupokea mabadiliko ya mfumo wa malipo ya kidijitali.

Aidha, uhamasishaji wa zoezi hilo umefanywa na Mrajis Msaidizi wa Mkoa wa Tabora, Peja Mhoja pamoja na Mrajis Msaidizi (Uhamasishaji), Ibrahim Kadudu, ambao wamekuwa mstari wa mbele kuwahamasisha wakulima kujiunga na mifumo rasmi ya kifedha ili kunufaika na malipo ya kisasa, salama na yenye tija.


Top News