Na Karama Kenyunko Michuzi Tv


KIJANA,Metson Frank (23) maarufu ‘Mkumbo’ anayeishi Goba Centre wilayani Ubungo amehikumiwa kifungo cha maisha jela baada ya kupatikana na hatia ya kosa la kumlawiti mtoto mwenye umri wa mwaka mmoja na miezi 10.

Hukumu hiyo ya kesi ya jinai namba 28576 ya mwaka 2026 imesomwa Jana ya na Hakimu Mkazi Mwandamizi, Tumsifu Barnabas wa Mahakama Wilaya ya Ubungo.

Kabla ya kusomwa kwa hukumu hiyo, Hakimu Barnabas aliuliza upande wa mashtaka kama walikuwa na lolote la kusema ndipo Wakili wa Serikali Mkuu, Flora Massawe akisaidiana na Wakili wa Serikali Mwandamizi, Agatha Lumato na Wakili wa Serikali, Clemence Mango waliomba mahakama itoe adhabu kali kwa mujibu wa sheria ili iwe fundisho kwa watu wengine wanaofanya ukatili kwa watoto

"Baada ya kusikiliza ushahidi wa pande zote na kufanya uchambuzi wa kina wa ushahidi uliowasilishwa, mahakama unamtia hatiani mshtakiwa kwa kosa la kulawiti kinyume na kifungu cha 154(1)(a)(2) cha Sheria ya Kanuni za Adhabu, Sura ya 16, Marejeo ya mwaka 2023". Alisema Hakimu

Akisoma hukumu huyo Hakimu Barnabas alisema ushahidi wa mashahidi nane na vielelezo vitatu vilivyowasilishwa mahakamani hapo na upande wa mashtaka umeweza kuthibitisha pasipo kuacha shaka kuwa mshtakiwa alitenda kosa hilo.

Amesema, katika hati ya mashataka ilidaiwa Septemba 10, 2025 majira ya usiku mshitakiwa ambaye ni baba wa kufikia wa mtoto huyo, alitenda kitendo hicho akiwa amelala naye katika chumba kimoja.

Hakimu alisema katika maelezo ya onyo ya mshtakiwa yaliyowasilishwa mahakamani hapo yalidai mshtakiwa alikiri kufanya kitendo hicho kwa kuwa mke wake ambaye ni mama wa mtoto aliyefanyiwa ukatili alikuwa ni mjamzito na hivyo alipata hamu ya ghafla.

Iliendelea kuelezwa kuwa mbali na kumlawiti mtoto huyo, mshtakiwa pia alimpiga na kumchapa kwa waya wa umeme ili asipige kelele wala kulia wakati akimfanyia kitendo hicho hali ambayo ilimuachia majeraha mbalimbali yaliyomlazimu kulazwa katika chumba cha wagonjwa mahututi (ICU) kwa muda mrefu.

Aliendelea kueleza kuwa baada ya matibabu, mtoto alipoteza uwezo wa kuona na kuongea.

Akiendelea kuchambua ushahidi wa mashahidi mbalimbali Hakimu Barnabas alieleza kuwa, katika ushahidi wake mama wa mtoto, alidai siku ya tukio walikuwa nyumbani kwa wazazi wa mwanaume eneo la Goba.

Alidai kuwa kutokana na hali yake ya ujauzito, alikwenda kulala huku mume wake akimuomba alale na mtoto huyo katika chumba kingine.

Asubuhi iliyofuata, alibaini kuwa katika chumba alichokuwa amelala mtoto kulikuwa na kinyesi na mtoto alionekana kama anaharisha.

Ilidaiwa kuwa Frank alimweleza hali hiyo mama yake mzazi ambaye walikuwa wanaishi naye, na baada ya kuona mtoto anaendelea kuharisha walimnunulia dawa za kuzuia kuharisha, lakini hali yake iliendelea kuwa mbaya.

Baada ya siku nne, walimpeleka mtoto katika Hospitali ya Taifa Muhimbili akiwa amezimia na kulazwa katika chumba cha wagonjwa mahututi (ICU).

Ilielezwa kuwa uchunguzi wa awali uliofanywa na madaktari ulibaini kuwa mtoto huyo huenda alikuwa amefanyiwa kitendo cha ukatili, kutokana na hali hiyo, madaktari walitoa taarifa katika Kituo cha Polisi Gogoni.

Ilidaiwa askari walifika hospitalini na kuanza uchunguzi mara moja na baada ya uchunguzi Frank alikamatwa nyumbani kwake Goba kwa tuhuma za kumlawiti mtoto huyo.

Hakimu alisema upande wa jamhuri ulihitimisha ushahidi wake na mshitakiwa alikutwa na kesi ya kujibu na katika utete zake alidai kuwa hata yeye alishangaa kuona mtoto ameamka akiwa anaharisha.

Alidai alitoa taarifa kwa watu wa karibu ambao walimshauri mtoto apelekwe hospitali ya Taifa ya Muhimbili na kwamba baada ya siku tatu alishangaa kukamatwa na polisi kuhusiana na tukio hilo.


Kampuni ya usafiri wa mtandao ya Bolt Tanzania jana iliwapokea wanafunzi kutoka programu ya Oasis Summer Camp 2026 katika Kituo cha Huduma kwa Madereva (Driver Engagement Centre – DEC) jijini Dar es Salaam, ikiwa ni sehemu ya ziara ya mafunzo iliyolenga kuwajengea uelewa kuhusu teknolojia, ubunifu na usalama katika matumizi ya huduma za usafiri wa kidijitali.

Ziara hiyo, iliyoandaliwa kwa ushirikiano na Oasis Village Club, iliwapa wanafunzi wa shule za msingi fursa ya kujionea kwa karibu namna makampuni ya kidijitali yanavyobadilisha huduma za usafiri na kuimarisha viwango vya usalama kwa madereva na abiria.

Katika mafunzo hayo, wanafunzi walitambulishwa baadhi ya zana za usalama zinazotumiwa na Bolt, ikiwemo mfumo wa kushirikisha taarifa za safari (Trip Sharing), ufuatiliaji wa safari kwa wakati halisi (Ride Tracking), huduma ya msaada wa dharura, uthibitishaji wa madereva pamoja na mifumo ya huduma kwa wateja inayoongeza uwajibikaji na uwazi katika kila safari.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Meneja wa Nchi wa Mawasiliano ya Bolt Tanzania, Gilbert Ginono, alisema kampuni inaamini kuwa kuwawezesha vijana kupitia elimu ni uwekezaji muhimu kwa mustakabali wa taifa.

"Tunaamini elimu ni miongoni mwa nyenzo muhimu zinazowawezesha vijana kuelewa namna teknolojia inavyoweza kubadilisha simulizi la changamoto zinazozikabili jamii zetu. Kupitia ziara kama hizi, wanafunzi hupata fursa ya kujifunza kwa vitendo kuhusu ubunifu wa Bolt unaowezesha madereva na abiria kusafiri kwa usalama.

Tunatarajia kuendeleza ushirikiano na shule pamoja na vyuo vikuu ili kuwaonesha namna teknolojia ilivyoboresha usalama wa usafiri leo ukilinganisha na miaka kumi iliyopita, ambapo kusafiri usiku kulikuwa na hofu kubwa zaidi na abiria hawakuwa na njia rahisi za kuthibitisha madereva au kushirikisha taarifa za safari zao na wapendwa wao."

Programu ya Oasis Summer Camp imeendelea kujizengea sifa kwa kuwapatia wanafunzi kutoka shule mbalimbali za Dar es Salaam fursa ya kutembelea taasisi na sekta tofauti, hatua inayowawezesha kupata maarifa na uzoefu wa vitendo nje ya mazingira ya darasani.

Bolt Tanzania imesisitiza kuwa itaendelea kuunga mkono mipango inayokuza matumizi salama ya teknolojia, uelewa wa masuala ya usalama pamoja na ubunifu kwa wanafunzi wa shule na vyuo vikuu, ikiwa ni sehemu ya kuandaa kizazi kijacho kwa uchumi wa kidijitali.



Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mheshimiwa Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesisitiza kuwa bado kuna fursa nyingi kwa taasisi za kifedha za ndani kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Rais Dkt. Mwinyi alitoa kauli hiyo jana alipokutana na ujumbe wa Absa Bank Tanzania, ukiongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wake, Bw. Obeid Laiser, aliyefanya ziara ya heshima Ikulu Zanzibar.

Amesema Serikali iko tayari kushirikiana kwa karibu na benki za ndani zinazodhihirisha dhamira ya kusaidia jitihada za maendeleo, hususan katika utekelezaji wa miradi ya kimkakati ya kiuchumi na kijamii katika sekta mbalimbali.

Rais Dkt. Mwinyi aliipongeza Absa Bank Tanzania kwa utayari wake wa kushirikiana na Serikali na kuchangia maendeleo ya Zanzibar. Aidha, alieleza kuwa Serikali imeimarisha mifumo ya kufadhili miradi ya maendeleo kwa kupanua vyanzo vya fedha nje ya bajeti ya kawaida, hatua inayolenga kuharakisha utekelezaji wa miradi na kuongeza ufanisi.

Rais aliwahakikishia viongozi wa benki hiyo kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na taasisi za kifedha katika kurahisisha utekelezaji wa miradi mikubwa ya maendeleo kupitia mikopo na mipango mingine ya kifedha.

Kwa upande wake, Bw. Obeid Laiser alishukuru Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa ushirikiano wake wa kudumu na benki hiyo na kumpongeza Rais Dkt. Mwinyi kwa uongozi wake uliosababisha maendeleo makubwa Zanzibar. Alisisitiza tena dhamira ya Absa Bank Tanzania kuendeleza ushirikiano na Serikali katika kusaidia utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo kwa manufaa ya wananchi na uchumi wa Zanzibar.

Bw. Laiser pia alieleza mchango wa Absa katika uchumi wa Zanzibar, akibainisha ueneaji na athari zake kupitia utoaji wa huduma za kifedha kwa watu binafsi, wafanyabiashara na mashirika makubwa.

Katika taarifa iliyotolewa baada ya mkutano huo, Bw. Laiser alieleza shukrani za benki kwa Serikali ya Zanzibar kwa kuunda mazingira wezeshi ya biashara na uwekezaji.

“Tunajivunia kupata fursa ya kukutana na Mheshimiwa Rais Hussein Ali Mwinyi na kujadili safari ya maendeleo ya kipekee ya Zanzibar. Kama mshirika wa kifedha anayeaminika, Absa itaendelea kujitolea kusaidia matarajio ya wananchi wa Zanzibar kupitia upatikanaji wa fedha, urahisishaji wa uwekezaji, ukuzaji wa ujasiriamali na suluhisho bunifu za kibenki zinazochangia katika ukuaji endelevu wa uchumi.

Absa inahudumia zaidi ya wateja 11,000 Zanzibar, inasimamia amana zinazozidi TZS bilioni 136 na imekopesha zaidi ya TZS bilioni 64 kwa watu binafsi, biashara ndogo na za kati pamoja na makampuni makubwa yanayofanya kazi katika sekta kuu za uchumi ikiwemo utalii, hoteli, biashara na uchuuzi,” alisema Bw. Laiser.

Bw. Laiser pia alisisitiza mchango wa Absa nje ya huduma za kibenki kupitia miradi ya uwajibikaji wa kijamii, ikiwemo kusaidia afya ya mama na mtoto chini ya mpango wa Uzazi ni Maisha, unaotekelezwa kwa ushirikiano na AMREF Health Africa na Wizara ya Afya Zanzibar. Kupitia mpango huu, Absa imechangia kuboresha upatikanaji wa vifaa muhimu vya kitabibu na kuimarisha huduma salama za kujifungua kwa akina mama na watoto wachanga Zanzibar.

Absa Bank Tanzania itaendelea kujitolea kwa dhima yake ya Kuimarisha Kesho ya Afrika, pamoja… hadithi moja kwa wakati, na kusaidia ustawi wa muda mrefu na mafanikio ya wananchi wa Zanzibar na Tanzania kwa ujumla.

Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Obedi Laiser (kushoto), akimkabidhi Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi (kulia), tuzo ya kumbukumbu kama ishara ya kuthamini ushirikiano imara kati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na sekta ya fesha pamoja na mageuzi makubwa ya kiuchumi visiwani humo. Ilikuwa wakati wa ziara ya Mkurugenzi huyo pamoja na ujumbe wake, Ikulu, mjini Zanzibar, juzi.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, akizungumza na ujumbe kutoka Benki ya Absa Tanzania, ulioongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wake, Bw, Obedi Laiser (wa tano kushoto), ulipomtembelea Ikulu, Zanzibar juzi. Bw. Laiser alitoa shukurani za benki kutokana na ushirkiano uliopo kati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na sekta za kibenki nchini pamoja na mageuzi makubwa ya kiuchumi yanayofanyika visiwani humo.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi (Katikati), akipiga picha ya kumbukumbu na ujumbe kutoka Benki ya Absa Tanzania, ulioongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wake, Bw, Obedi Laiser (kulia kwake), ulipomtembelea Ikulu, Zanzibar juzi. Wakati wa mazungumzo yao, Bw. Laiser alitoa shukurani za benki kutokana na ushirkiano uliopo kati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na sekta za kibenki nchini pamoja na mageuzi makubwa ya kiuchumi yanayofanyika visiwani humo. (PICHA NA IKULU)


NA DENIS MLOWE ,IRINGA

SHIRIKA la Hand in Hand Eastern Africa Tanzania (HIHEA) limezindua rasmi utekelezaji wa mradi wa Inua 2 mkoani Iringa, likitarajia kuwafikia wananchi 8,000 kupitia mafunzo ya ujasiriamali, usimamizi wa biashara, na uboreshaji wa shughuli za uzalishaji katika sekta za kilimo na ufugaji.

Akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi iliyofanyika katika Ukumbi wa Gentle Hills mjini Iringa, Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Iringa, Elia Luvanda alisema ujio wa shirika hilo unaongeza nguvu katika juhudi za serikali za kuharakisha maendeleo ya kiuchumi kwa wananchi wa mkoa huo.

Luvanda alisema serikali ina matarajio makubwa kwamba Hand in Hand itasaidia kuimarisha vikundi vya wananchi kwa kuwajengea uwezo katika maeneo mbalimbali ikiwemo uandaaji wa mipango ya biashara, uongozi wa vikundi, utunzaji wa kumbukumbu na usimamizi wa shughuli za uzalishaji.

Alieleza kuwa mafunzo hayo yatawawezesha wanufaika kuwa tayari kupata huduma za kifedha kutoka taasisi mbalimbali pamoja na mikopo ya asilimia kumi inayotolewa na halmashauri kwa vijana, wanawake na watu wenye ulemavu.

“Tunawakaribisha na tuko tayari kutoa ushirikiano wote unaohitajika na serikali imewaelekeza viongozi wa ngazi zote kuhakikisha shirika hili linapata mazingira mazuri ya kufanya kazi na kuwafikia wananchi waliokusudiwa,” alisema

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Hand in Hand Eastern Africa Tanzania, Jane Richard Sabuni, alisema shirika hilo limetenga bajeti ya bilioni 2.8 kwa ajili ya utekelezaji wa mradi huo, ambapo zaidi ya asilimia 70 ya fedha hizo zitaelekezwa moja kwa moja kwa shughuli za kuwawezesha walengwa.

Sabuni alisema mradi huo unalenga kuongeza kipato cha kaya kwa kiwango kikubwa kupitia biashara endelevu, kilimo chenye tija, ufugaji na shughuli nyingine za uzalishaji zitakazochaguliwa na wanufaika kulingana na mazingira yao.

Alifafanua kuwa kuwajengea uwezo wanufaika hakutakuwa kwa njia ya mafunzo ya darasani pekee, bali kutahusisha mashamba darasa, wakulima na wafugaji wa mfano, pamoja na ushiriki wa wataalamu wa sekta mbalimbali watakaowasaidia wananchi kuongeza tija katika shughuli zao.

Sabuni alisema Hand in Hand haitatoa mikopo ya fedha moja kwa moja kwa wanufaika, bali itakuwa kiungo kati ya wafanyabiashara wadogo na taasisi zinazotoa huduma za kifedha baada ya kuhakikisha wamepata mafunzo, wameandaa mipango ya biashara na kutimiza masharti yanayohitajika.

“Tunalenga kuwafikia wananchi 8,000 na kuona maisha yao yanabadilika kupitia ongezeko la kipato, biashara endelevu na fursa za ajira. Mafanikio ya mradi huu yatatokana pia na ushiriki wa wananchi wenyewe katika kutumia maarifa watakayopata,” alisema.

Meneja wa Hand in Hand Tawi la Iringa, Amos Kasanga, alisema utekelezaji wa awamu ya kwanza ya mradi huo utaanza katika Manispaa ya Iringa na Wilaya ya Iringa, ukihusisha kata 12 na walengwa wapatao 4,000.

Alisema baada ya kukamilika kwa awamu hiyo, shirika litapanua shughuli zake na kufikia maeneo mengine ikiwemo Wilaya ya Kilolo pamoja na kuongeza idadi ya kata zitakazoshiriki katika mpango huo.

Kasanga alieleza kuwa wanufaika watapitia mafunzo ya miezi 11 yatakayojumuisha elimu ya biashara, utambuzi wa fursa za kiuchumi, usimamizi wa shughuli za uzalishaji na namna ya kuunganisha bidhaa zao na masoko.
Aliongeza kuwa uteuzi wa wanufaika utafanyika kupitia vikundi vilivyopo katika vijiji na kata mbalimbali, ambapo shirika litashirikiana na viongozi wa serikali za mitaa kubaini mahitaji yaliyopo na kutoa msaada unaolenga kuimarisha shughuli za kiuchumi za wananchi.

Kupitia mradi huo, Hand in Hand inatarajia kuchochea ukuaji wa uchumi wa kaya, kuongeza ajira na kupunguza umaskini kwa kuimarisha uwezo wa wananchi kushiriki kikamilifu katika shughuli za uzalishaji na biashara zenye tija.






Na Janeth Raphael MichuziTv - Bungeni Dodoma 

Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba, amesema kuwa Shilingi ya Tanzania ndiyo fedha halali ya malipo ndani ya nchi, akisisitiza kuwa matumizi yake yanalindwa na Katiba pamoja na sheria za nchi. Amesema Serikali itaendelea kuhakikisha kuwa taratibu na sheria zinazohusu matumizi ya sarafu ya taifa zinafuatwa ili kuimarisha uchumi wa ndani.

Dkt. Nchemba ametoa kauli hiyo Bungeni jijini Dodoma leo wakati wa kipindi cha Maswali kwa Waziri Mkuu alipokuwa akijibu swali lililoulizwa na Mbunge wa Viti Maalum, Suma Fyandomo. 

Katika majibu yake, Waziri Mkuu alieleza kuwa Shilingi ya Tanzania ndiyo chombo rasmi cha kufanya malipo katika shughuli mbalimbali za kiuchumi zinazofanyika ndani ya mipaka ya nchi.

Amesisitiza kuwa nafasi ya Shilingi ya Tanzania kama fedha halali ya malipo si suala la hiari, bali ni matakwa ya kisheria yanayopaswa kuheshimiwa na wadau wote wa uchumi, wakiwemo wafanyabiashara, taasisi na wananchi kwa ujumla. Kwa mujibu wa Waziri Mkuu, matumizi ya sarafu ya taifa yana mchango mkubwa katika kulinda uthabiti wa mfumo wa fedha na kuimarisha uchumi wa nchi.

“Shilingi ya Kitanzania ndiyo malipo halali ndani ya nchi yetu, na hili ni jambo la kikatiba na ni jambo la kisheria,” alisema Dkt. Nchemba wakati akijibu swali hilo mbele ya Bunge.

Kauli hiyo imekuja katika kipindi ambacho kumekuwepo mijadala kuhusu matumizi ya fedha za kigeni katika baadhi ya huduma na shughuli za biashara nchini. Serikali imekuwa ikisisitiza umuhimu wa kuzingatia sheria na miongozo inayotaka malipo ya ndani kufanyika kwa kutumia sarafu ya Tanzania isipokuwa pale ambapo sheria au kanuni husika zinatoa ruhusa maalumu.

Aidha, msimamo huo wa Serikali unalenga kuendelea kuimarisha hadhi ya Shilingi ya Tanzania, kuongeza imani kwa sarafu ya taifa na kuchochea ukuaji wa uchumi wa ndani. Serikali imeeleza kuwa itaendelea kutoa elimu na kusimamia utekelezaji wa sheria ili kuhakikisha matumizi ya Shilingi ya Tanzania yanaendelea kuwa msingi mkuu wa miamala ya kifedha nchini.



Jane Mwakyoma, Juni 25, 2026,  Rukwa.

TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Rukwa imeendesha mafunzo maalumu kwa wasimamizi wa miradi ya maendeleo kutoka halmashauri zote nne za mkoa huo, yakilenga kuimarisha uwajibikaji, uwazi na ufanisi katika utekelezaji wa miradi.

Akifungua mafunzo hayo yaliyofanyika katika Halmashauri ya wilaya ya Sumbawanga Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Charles Makongoro Nyerere amewataka wasimamizi wa miradi kutumia elimu wanayopewa kama nyenzo ya kuimarisha usimamizi wa miradi inayogusa maisha ya wananchi moja kwa moja.

Amesema utekelezaji wa miradi bila kuzingatia sheria, kanuni za manunuzi na taratibu za ujenzi unaweza kusababisha migogoro hasara kwa Serikali na kuchelewesha huduma muhimu zinazotarajiwa na wananchi.

“Miradi ya maendeleo ni matumaini ya wananchi. Ni wajibu wa kila msimamizi kuhakikisha fedha za umma zinatumika kwa uadilifu na miradi inakamilika kwa viwango vinavyotakiwa na kwa wakati,” amesema.

Kwa upande wake Kamanda wa TAKUKURU Mkoa wa Rukwa Mzalendo Widege amesema mafunzo hayo yanalenga kujenga uelewa wa pamoja kati ya wasimamizi na wafuatiliaji wa miradi ili kuzuia mianya ya ubadhirifu, kuongeza uwajibikaji na kuhakikisha miradi inawanufaisha wananchi kama ilivyokusudiwa.

Pia amesema usimamizi bora wa miradi ni msingi wa maendeleo endelevu kwani huongeza thamani ya fedha za umma na kuimarisha imani ya wananchi kwa taasisi za Serikali.

Kwa niaba ya washiriki wa mafunzo hayo Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga Missana Kwangura, ameishukuru TAKUKURU kwa kuandaa mafunzo hayo ambayo amesema yamewapa maarifa muhimu yatakayosaidia kuongeza ufanisi katika usimamizi wa miradi ya maendeleo.

Kwangura amesema washiriki wamejipatia uelewa mpana kuhusu wajibu wao katika kusimamia rasilimali za umma na kuahidi kuyafanyia kazi mafunzo waliyoyapata kwa kuzingatia sheria, kanuni ,miongozo na taratibu zote za usimamizi wa miradi.

Mpango huo wa TAKUKURU unatarajiwa kusaidia kupunguza malalamiko yanayohusiana na utekelezaji wa miradi ya maendeleo, kuimarisha uwazi katika matumizi ya rasilimali za umma na kuhakikisha kila shilingi ya maendeleo inaleta matokeo chanya kwa wananchi wa Mkoa wa Rukwa.


Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) inawakaribisha walipakodi wote nchini kushiriki matembezi na mbio za Shukrani kwa Mlipakodi kuelekea Tuzo ya Rais kwa Mlipakodi bora na Maadhimisho ya miaka 30 ya TRA 

 Karibuni walipakodi wote na watanzania kwa ujumla siku ya Traehe 27 Juni, 2026 kuanzia saa 12 Asubuhi.‘Miaka 30 ya TRA, Kulipa kodi ni Uzalendo na Ushujaa kwa Maendeleo na kujitegemea kwa Taifa letu’’

#MbiozashukraniTRA #Miaka30yaTRA #TuzozaRaiskwamlipakodi


Na Mwandishi Wetu, Kigoma

Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC), Mohamed Salum, amesema mabaharia wana mchango mkubwa katika ukuaji wa uchumi wa taifa kutokana na nafasi yao muhimu katika usafirishaji wa bidhaa zinazoingia na kutoka nchini.

Salum aliyasema hayo wakati akifungua  Warsha  kuelekea kilele cha Maadhomisho  cha Siku ya 16 ya Mabaharia Duniani yanayofanyika mkoani Kigoma, ambapo alieleza kuwa takribani asilimia 80 ya bidhaa zinazoingia nchini husafirishwa kwa njia ya maji na kufikishwa kwa watumiaji kupitia juhudi za mabaharia.

Alisema mchango wa mabaharia hauishii kwenye usafirishaji wa bidhaa pekee, bali pia una athari kubwa katika maendeleo ya kijamii na kiuchumi kwa kuhakikisha mnyororo wa biashara unaendelea kufanya kazi kwa ufanisi.

“Mabaharia ni nguzo muhimu ya uzalishaji na maendeleo ya uchumi. Bila wao, shughuli nyingi za biashara na usafirishaji zingekwama,” alisema Salum.

Aliongeza kuwa TASAC itaendelea kusimamia na kuratibu sekta ya mabaharia kwa kuhakikisha viwango vya kitaaluma na usalama vinazingatiwa ili mabaharia wa Tanzania waendelee kuwa na ushindani katika soko la ajira duniani.

Akizungumzia changamoto zinazowakabili mabaharia, Salum alisema migogoro inayoendelea katika baadhi ya maeneo duniani, ikiwemo mvutano kati ya Iran na Israel unaohusisha njia muhimu za usafiri wa majini, imeongeza hatari kwa mabaharia wanaotekeleza majukumu yao katika maeneo hayo.

Alibainisha kuwa Tanzania tayari imepoteza mmoja wa mabaharia wake kutokana na changamoto zinazotokana na mazingira ya migogoro, jambo linalosisitiza umuhimu wa kuimarisha ulinzi na usalama wa wafanyakazi hao wanapokuwa kazini.

“Tunahitaji kuona juhudi zaidi za kimataifa katika kulinda mabaharia, kwa sababu wao ndiyo uti wa mgongo wa sekta ya usafirishaji wa majini duniani,” alisema.

Aidha, alisisitiza umuhimu wa mabaharia kushiriki kikamilifu katika kulinda mazingira ya bahari na maziwa, akieleza kuwa mfumo wa ikolojia wa maeneo hayo una umuhimu mkubwa kwa maisha ya viumbe hai na ustawi wa jamii zinazotegemea rasilimali za maji.

Salum pia alitaja Ziwa Tanganyika kuwa moja ya nyenzo muhimu za uchumi wa Tanzania kutokana na kuunganisha Tanzania na nchi nne jirani, hivyo kutoa fursa kubwa za biashara, usafiri na maendeleo kwa wananchi wa ukanda huo.

Aliwahimiza mabaharia kuendelea kufanya kazi kwa weledi na uzalendo huku akiihakikishia jamii ya mabaharia kuwa Serikali kupitia TASAC itaendelea kuthamini mchango wao, kuimarisha usalama wao na kuboresha mazingira ya kazi ili sekta hiyo iendelee kuwa kichocheo muhimu cha ukuaji wa uchumi wa taifa.

Mkurugenzi Mkuu wa TASAC Mohamed Salum akizungumza wakati akifungua Warsha ya Mabaharia kuelekea Kilele cha Maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani Mjini Kigoma
Mkuu wa Chuo cha DMI Profesa Tumaini Gurumo akizungumza katika Warsha ya Mabaharia katika Maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani mkoani Kigoma.



Matukio katika picha katika Warsha ya Mabaharia mkoani Kigoma

-Zoezi la Uokoaji Kigoma Laonesha Uwekezaji wa Serikali Katika Usalama Majini


Na Mwandishi Wetu, Kigoma

Mkuu wa Wilaya ya Kigoma, Rashid Chuachua, amesema kuwa usalama wa mabaharia na vyombo vya usafiri katika Ziwa Tanganyika ni jambo la msingi linalopaswa kupewa kipaumbele ili ziwa hilo liendelee kuwa nguzo muhimu ya uzalishaji na maendeleo ya uchumi wa Mkoa wa Kigoma na Taifa kwa ujumla.

Chuachua alitoa kauli hiyo wakati wa zoezi la majaribio ya utafutaji na uokoaji lililoshirikisha vikosi vya ulinzi na usalama pamoja na Boti ya Utafutaji na Uokoaji ya Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC), lililofanyika katika Bandari ya Kibilizi mkoani Kigoma.

Alisema kuwa kuimarishwa kwa mifumo ya uokoaji na usalama majini kutasaidia kupunguza madhara yanayotokana na ajali za vyombo vya majini, huku akisisitiza umuhimu wa kuongeza ukaguzi wa mara kwa mara wa vyombo hivyo ili kuzuia majanga yanayosababishwa na makosa ya kibinadamu.

“Ziwa Tanganyika ni rasilimali muhimu ya kiuchumi. Ili liendelee kutoa mchango wake kikamilifu, ni lazima tuhakikishe mabaharia na vyombo vya usafiri vinakuwa salama wakati wote,” alisema Chuachua.

Aidha, alisema maadhimisho ya Siku ya Mabaharia pamoja na maonesho ya zoezi la uokoaji yanaonesha dhamira ya Serikali katika kuwekeza kwenye vifaa na miundombinu ya kisasa ya uokoaji kwa lengo la kulinda maisha ya wananchi wanaotumia usafiri wa majini.

Chuachua pia aliwataka mabaharia na waendeshaji wa vyombo vya majini kuhakikisha wanazingatia taarifa za hali ya hewa zinazotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) kabla ya kuanza safari zao ili kujiepusha na hatari zinazoweza kujitokeza kutokana na mabadiliko ya hali ya hewa.

“Ni muhimu kwa mabaharia kufuatilia utabiri wa hali ya hewa kabla ya kuanza safari. Hii itasaidia kulinda maisha yao pamoja na mizigo inayosafirishwa,” alisisitiza.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa TASAC, Mohamed Salum, alisema kuwa Boti ya Utafutaji na Uokoaji iliyowekwa katika Ziwa Tanganyika ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kuimarisha usalama wa wananchi wanaosafiri kwa njia ya maji na kuhakikisha huduma za uokoaji zinapatikana kwa haraka pale majanga yanapotokea.

Alisema TASAC itaendelea kusimamia viwango vya usalama majini na kutoa huduma bora kwa mabaharia pamoja na wadau wengine wa sekta ya usafiri wa majini nchini.

“Tumeleta boti hii kwa lengo la kuhakikisha wananchi wanaopata majanga majini wanapata msaada wa haraka.Pia tunaendelea kuhimiza mabaharia kutoa taarifa mapema wanapokumbana na changamoto ili hatua za uokoaji ziweze kuchukuliwa kwa wakati,” alisema Salum.

Zoezi hilo limeelezwa kuwa sehemu ya maandalizi ya kuimarisha uwezo wa kukabiliana na dharura majini na kuongeza uelewa wa wadau kuhusu umuhimu wa usalama katika sekta ya usafiri wa majini, hususan katika Ziwa Tanganyika ambalo ni moja ya njia muhimu za usafirishaji na biashara nchini.
Mkuu wa Wilaya ya Kigoma Rashid Chuachua akizungumza wakati zoezi la jaribio la uokoaji lililofanyika katika Bandari ya Kibilizi ikiwa ni maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani yanayoendelea mkoani Kigoma.
Mkurugenzi Mkuu wa TASAC Mohamed Salum akitoa maelezo kuhusiana na zoezi la uokoaji lililofanyika katika Bandari ya Kibilizi katika maadhimisho ya 16 ya Siku Mabaharia Duniani yanayoendelea mkoani Kigoma.
Mkurugenzi wa Usalama wa Usafiri na Mazingira wa Wizara ya Uchukuzi Stella Katondo akizungumza kuhusiana na serikali ilivyowekeza katika uokoaji katika majanga ya usafiri wa majini kwenye maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani yanayoendelea mkoani Kigoma.

Baadhi ya matukio ya jaribio la uokoaji ya mmoja wa afisa aliyejirusha ziwani ili kupata msaada wa kuokolewa.


 

Bodi ya Usimamizi wa Mfumo wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) imeanza rasmi utekelezaji wa maagizo yaliyotolewa na Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba, ya kuimarisha usimamizi wa Mfumo wa Stakabadhi za Ghala na kuhakikisha changamoto zinazojitokeza katika utekelezaji wake zinatatuliwa bila kurudi kwenye biashara holela ya mazao.

Akitoa taarifa baada ya kutembelea mikoa ya Pwani, Lindi, Mtwara, Ruvuma, Morogoro na Iringa ikiwa ni utekelezaji wa maagizo hayo aliyoyatoa kwenye maadhimisho ya miaka 20 ya Bodi hiyo Mei 19, 2026 jijini Dodoma, Mkurugenzi Mtendaji wa WRRB, Bw. Asangye Bangu, amesema katika ziara hiyo amekutana na viongozi wa mikoa, wilaya na Kamati za Usimamizi wa Mfumo wa Stakabadhi za Ghala na kujionea namna mfumo huo unavyotekelezwa kwenye zao la ufuta.

“Nimeridhishwa na namna serikali za mikoa zinavyoendelea kushirikiana na WRRB katika kuhakikisha mfumo unasimamiwa vizuri. Viongozi wote tuliokutana nao wameonesha utayari mkubwa wa kusimamia utekelezaji wa mfumo huu na kushughulikia changamoto zinazojitokeza,” amesema.

Amesema moja ya maelekezo makubwa yaliyotolewa na Waziri Mkuu ni kuhakikisha changamoto zinazojitokeza katika mfumo huo hazitumiki kama sababu ya kurejea katika biashara holela ya mazao, bali zitafutiwe ufumbuzi kwa wakati.

Kwa mujibu wa Bw. Bangu, changamoto zilizotajwa na Waziri Mkuu zinahusisha miundombinu ikiwamo ujenzi wa maghala, matengenezo ya barabara na uwepo wa mazingira bora ya kurahisisha usafirishaji wa mazao yanayopitia katika mfumo huo. Amesema WRRB imeweka mikakati mahsusi ya kuhakikisha ubora wa mazao unaimarishwa kwa kushirikiana na wakuu wa mikoa na wilaya ili bidhaa zote zinazopelekwa maghalani zikidhi viwango vinavyotakiwa.

“Tumewaelekeza waendesha maghala kuzingatia kikamilifu miongozo iliyotolewa na taasisi husika. Kwa sasa zao lililo sokoni ni ufuta na tayari miongozo ya utekelezaji imetolewa na COPRA,” amesema.

Kuhusu upungufu wa maghala, Bw. Bangu amesema tayari WRRB imeanza mazungumzo na halmashauri mbalimbali ili kuona namna ya kutumia fursa ya uwekezaji katika miundombinu ya maghala ambayo itaongeza ufanisi wa mfumo huo na kuwafikisha wakulima karibu zaidi na minada.

Kadhalika, amesema WRRB kwa kushirikiana na COPRA pia imeanza kuangalia uwezekano wa kuongeza mazao mengine kwenye mfumo ikiwamo karanga, njugu mawe na choroko ili kuongeza idadi ya wanufaika.

Akizungumzia changamoto ya mdororo wa bei, Bangu amesema wananchi wamekuwa wakilinganisha bei za sasa na zile za miaka mitatu iliyopita bila kuzingatia mabadiliko ya soko la dunia, hivyo WRRB imeendelea kutoa elimu kuhusu mwenendo wa bei katika masoko ya kimataifa.

Pia amesema baadhi ya maeneo yamekumbwa na upungufu wa uzalishaji kutokana na mabadiliko ya hali ya hewa na ukosefu wa mbegu bora, na kwamba WRRB imeanza mazungumzo na Jeshi la Magereza ili kutumia mashamba yake kuongeza uzalishaji wa mbegu.

“Niwahakikishie wananchi kuwa mfumo huu ni imara na tunaendelea kutatua changamoto zote zinazojitokeza. Tukishirikiana na wadau wote, tutamkomboa mkulima wa Tanzania na kuhakikisha anapata thamani halisi ya mazao yake,” alisema.

Na Mwandishi Wetu - Dodoma

SERIKALI imesema imejipanga kikamilifu kukabiliana na madhara yanayoweza kusababishwa na hali ya El Niño kufuatia tahadhari iliyotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA).

Akizungumza hii leo 24 Juni, 2026 wakati wa ufunguzi wa kikao cha wadau wa usimamizi wa maafa, Mkurugenzi Msaidizi Sehemu ya Operesheni na Uratibu kutoka Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) Kanali Selestine Masalamado, amesema kuwa tayari Serikali imeandaa Rasimu ya Mpango wa Taifa wa Dharura ili kuimarisha maandalizi na hatua za kukabiliana na hali hiyo.

Amesema mpango huo unalenga kuhakikisha kunakuwa na uratibu madhubuti, utekelezaji wa hatua za mapema pamoja na kupunguza athari zinazoweza kujitokeza kwa wananchi, mali zao na miundombinu.

“Kikao hiki kinatoa fursa kwa wizara, taasisi, mikoa na wadau wengine kupitia rasimu hii kwa kina na kutoa maoni yatakayosaidia kupatikana kwa mpango shirikishi na unaotekelezeka,” amesema Kanali Masalamado

Ameongeza kuwa Serikali inathamini mchango wa wadau wote katika kuboresha mpango huo ili uwe mwongozo thabiti wa kuzuia, kujiandaa na kukabiliana na madhara ya El Niño.

Aidha, amewataka washiriki kushiriki kikamilifu katika majadiliano na kutoa mapendekezo yenye kujenga yatakayosaidia kulinda maisha ya wananchi na kuhakikisha huduma muhimu zinaendelea kutolewa hata wakati wa majanga.

Katika hatua za maandalizi, amesisitiza umuhimu wa kutoa elimu kwa umma kuhusu tahadhari za kuchukua, ikiwemo kuhama katika maeneo hatarishi na kuendelea na shughuli za kiuchumi katika maeneo salama.

Kwa mujibu wa Kanali Masalamado, kuna umuhimu wa kubaini maeneo salama kwa ajili ya makazi ya muda, pamoja na kuainisha maeneo hatarishi ili kuwezesha hatua za haraka za kukabiliana na maafa.

Sambamba na hilo, amesisitiza kuimarishwa kwa mifumo ya mawasiliano na utoaji wa tahadhari za mapema ili wananchi wapate taarifa sahihi kwa wakati.

“Ninazikumbusha mamlaka za mikoa na serikali za mitaa kuhakikisha kamati za usimamizi wa maafa katika ngazi zote zinatekeleza majukumu yao kikamilifu, huku ufuatiliaji ukiendelea kufanyika mara kwa mara,” amesisitiza

Ameongeza kuwa ni wajibu wa taasisi na mikoa kuhuisha au kuandaa mipango yao ya dharura kwa haraka ili Taifa liwe tayari kukabiliana na athari za El Niño endapo zitajitokeza.

















Na Janeth Raphael MichuziTv

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, ametoa wito kwa Watanzania kujenga utamaduni wa kufanya uchunguzi wa afya mara kwa mara ili kuwezesha ugunduzi wa mapema wa saratani, akisisitiza kuwa ugonjwa huo si hukumu ya kifo iwapo utabainika mapema na mgonjwa kupata matibabu stahiki.

Rais Samia ameyasema hayo leo wakati wa uzinduzi rasmi wa Jengo la Tiba ya Mionzi kwa Wagonjwa wa Saratani katika Kilimanjaro Christian Medical Centre mkoani Kilimanjaro Region, ambapo alieleza kuwa Serikali imeendelea kuwekeza katika sekta ya afya kwa lengo la kusogeza huduma muhimu karibu na wananchi.

Akihutubia wananchi, viongozi wa dini na wadau mbalimbali waliohudhuria hafla hiyo, Rais Samia alisema bado kuna haja kubwa ya kuondoa hofu na mitazamo isiyo sahihi kuhusu saratani, huku akisisitiza umuhimu wa uchunguzi wa mapema kama njia bora ya kuongeza nafasi za mafanikio ya matibabu.

“Saratani si hukumu ya kifo. Mtu akigundulika mapema na kufuata maelekezo ya wataalamu wa afya, ana nafasi kubwa ya kupona na kuendelea na maisha yake ya kawaida,” alisema Rais Samia.

Rais huyo alitoa rai maalum kwa wanaume kujitokeza kupima afya zao, hususan uchunguzi wa saratani ya tezi dume, akibainisha kuwa wengi huchelewa kufika hospitalini kutokana na hofu au kuona aibu, jambo linalochangia ugonjwa kugundulika ukiwa umefikia hatua za juu.

“Wanaume wasisite kwenda kupima. Ni muhimu kuchukua hatua mapema kabla ugonjwa haujasababisha madhara makubwa zaidi,” alisisitiza.

Kwa upande wa wanawake, Rais Samia alihimiza uchunguzi wa mara kwa mara wa saratani ya mlango wa kizazi na saratani ya matiti, akieleza kuwa hatua hiyo imekuwa miongoni mwa njia muhimu za kuokoa maisha ya wanawake wengi.

Mbali na wananchi, Rais Samia aliwataka wataalamu wa afya kuongeza juhudi katika utoaji wa elimu kwa umma kuhusu magonjwa yasiyoambukiza, ikiwemo saratani. Pia alipendekeza kuanzishwa kwa siku maalum za uchunguzi wa afya katika jamii ili kuwafikia wananchi wengi zaidi.

Aidha, alisisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya Serikali, taasisi za dini, wataalamu wa afya na vyombo vya habari katika kuelimisha umma kuhusu njia sahihi za kinga, uchunguzi na matibabu ya saratani.

Akizungumzia suala la imani na tiba, Rais Samia alisema ni muhimu wananchi kutambua kuwa huduma za afya za kitaalamu zina nafasi muhimu katika kuokoa maisha, huku akihimiza wagonjwa kutotegemea tiba zisizo na uthibitisho wa kisayansi.

“Imani na tiba vinaweza kwenda pamoja. Tunapaswa kutumia maarifa na wataalamu ambao wamewezeshwa kusaidia kuokoa maisha ya wananchi,” alisema.

Ufunguzi wa Jengo la Tiba ya Mionzi katika KCMC unatajwa kuwa hatua muhimu katika kuimarisha huduma za matibabu ya saratani nchini, huku ukitarajiwa kupunguza gharama na safari ndefu kwa wagonjwa waliokuwa wakilazimika kusafiri umbali mrefu kutafuta huduma hizo.

Mradi huo pia unalenga kuongeza upatikanaji wa huduma za kisasa za matibabu ya saratani, kuharakisha uchunguzi na matibabu ya wagonjwa, pamoja na kuboresha kwa ujumla huduma za afya katika ukanda wa Kaskazini mwa Tanzania.






Top News