Serikali imezindua Kielelezo cha Viwango vya Faida vya Dhamana za Serikali (Government Securities Yield Curve), hatua inayotarajiwa kuimarisha uwazi wa soko la fedha, kuongeza ufanisi wa maamuzi ya uwekezaji na kuvutia mitaji ya ndani na nje ya nchi.
Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania Bw. Emmanuel Tutuba, kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), amezindua Kielelezo hicho katika hafla iliyofanyika ukumbi wa mikutano wa Kilimanjaro, Benki Kuu ya Tanzania, jijini Dar es Salaam.
Bw. Tutuba alisema kupitia Kielelezo hicho wawekezaji wataweza kuona na kufuatilia mwenendo wa faida halisi katika soko la upili la Dhamana za Serikali, jambo litakalowasaidia kufanya maamuzi ya uwekezaji kwa kuzingatia taarifa sahihi na zinazoaminika.
‘‘Kielelezo hicho kitawawezesha wawekezaji wa ndani na wa kimataifa kulinganisha viwango vya faida vya Dhamana za Serikali ya Tanzania na fursa nyingine za uwekezaji ndani ya nchi, pamoja na masoko ya kikanda na kimataifa, hivyo kuongeza uwazi wa soko, kuvutia wawekezaji wa kigeni na kuimarisha ushindani wa soko la fedha nchini’’, alisema Bw. Tutuba.
Aidha Bw. Tutuba alisema Kielelezo hicho pia kitaakisi matarajio ya soko kuhusu ukuaji wa uchumi, mfumuko wa bei na mwelekeo wa sera ya fedha, hivyo kitakuwa nyenzo muhimu kwa Benki Kuu katika kuimarisha utekelezaji wa sera ya fedha inayotegemea viwango vya riba.
‘‘Soko letu limeshuhudia ukuaji mkubwa katika kipindi cha miaka 25, ambapo mwaka 2001, Dhamana za Serikali ambazo zilikuwa hazijaiva zilifikia shilingi bilioni 499, na kuongezeka mpaka kufikia shillingi trilioni 32.3 hivi sasa’’, alisema Bw. Tutuba.
Vilevile, alisema uthaminishaji wa Dhamana za Serikali zinazowasilishwa na mabenki ya biashara kama dhamana ya kupata mikopo kutoka Benki Kuu utafanyika kwa kutumia kielelezo hicho, hatua inayotarajiwa kuongeza usahihi na uwazi katika shughuli za kifedha.
‘‘Kwa upande wa sekta ya fedha, mabenki, mifuko ya hifadhi ya jamii, makampuni pamoja na wawekezaji binafsi watanufaika kwa kutumia taarifa za kielelezo hicho kama kiwango salama cha rejea katika kupanga viwango vya riba vya mikopo, mikopo ya nyumba, hatifungani za makampuni na bidhaa nyingine za uwekezaji’’, alifafanua Bw. Tutuba.
Bw. Tutuba aliwashukuru wadau wote wa soko kwa ushiriki wao ambao umeiwezesha Serikali kupata fedha za kutekeleza miradi ya maendeleo kupitia Dhamana za Serikali pamoja na kuanza utekelezaji wa Dira ya Taifa ya 2050.
Alisisitiza kuwa kuna umuhimu wa Benki Kuu na Serikali kwa ujumla kuendelea kutoa elimu ya uwekezaji ili kuhakikisha soko linaendelea kukua kwa kasi na kuongeza idadi ya wawekezaji kutoka 32,631 walioko sasa kwani idadi hiyo ni ndogo ikilinganishwa na idadi ya watu nchini.
Awali, akizungumza katika tukio hilo, Kamishna wa Idara ya Usimamizi wa Madeni, Wizara ya Fedha, Bw. Japhet Justine, alisema kuwa soko la hisa limeendelea kukua ambapo
katika mwaka wa fedha 2025/26, thamani ya miamala iliyofanyika ilikuwa zaidi ya shilingi trilioni 6.7.
Alisema soko hilo ni fursa muhimu katika kuelekea utekelezaji wa Dira 2050 ambayo sehemu kubwa ya utekelezaji wake inatarajiwa itokane na sekta binafsi kwa takribani asilimia 70 hususani katika upatikanaji wa kitaji.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE), Bw. Peter Nalitolela, alisema kuwa Kielelezo hicho kitaongeza miamala na ukwasi katika soko la dhamana na kuchochea maendeleo ya aina nyingine za mali zinazouzwa katika soko la hisa.
Alipongeza Benki Kuu ya Tanzania kwa kuchapisha Kanuni za Marekebisho ya Udhibiti wa Fedha za Kigeni za mwaka 2026 na uzinduzi wa Kielelezo hicho kuwa hatua hiyo itaimarisha zaidi mfumo wa fedha nchini na kuweka mazingira yatakayowezesha Tanzania kuwa na soko la mitaji lenye ufanisi, uwazi na ushindani.
Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akibonyeza kitufe kuashiria uzinduzi rasmi wa Kielelezo cha Viwango vya Faida vya Dhamana za Serikali (Government Securities Yield Curve), katika hafla iliyofanyika ukumbi wa mikutano wa Kilimanjaro, Benki Kuu ya Tanzania, jijini Dar es Salaam. Wanaoshuhudia ni Kamishna Idara ya Usimamizi wa Madeni, Wizara ya Fedha, Bw. Japhet Justine (wa tatu kushoto), Naibu Gavana, Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Dkt. Yamungu Kayandabila (wa pili kushoto) na Kaimu Kamishna wa Idara ya Uendelezaji wa Sekta ya Fedha, Wizara ya Fedha Bi. Dionisia Mjema. Kulia ni Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA), Nicodemas Mkama.
Meza kuu ikiongozwa na Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Bw. Emmanuel Tutuba, kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), wakifurahia baada ya kuzinduliwa rasmi kwa Kielelezo cha Viwango vya Faida vya Dhamana za Serikali (Government Securities Yield Curve), katika hafla iliyofanyika ukumbi wa mikutano wa Kilimanjaro, Benki Kuu ya Tanzania, jijini Dar es Salaam.
Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Bw. Emmanuel Tutuba, kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akizungumnza katika hafla ya uzinduzi wa Kielelezo cha Viwango vya Faida vya Dhamana za Serikali (Government Securities Yield Curve), iliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Kilimanjaro, Benki Kuu ya Tanzania, jijini Dar es Salaam.
Kamishna Idara ya Usimamizi wa Madeni, Wizara ya Fedha Bw. Japhet Justine, akizungumnza katika hafla ya uzinduzi wa Kielelezo cha Viwango vya Faida vya Dhamana za Serikali (Government Securities Yield Curve), iliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Kilimanjaro, Benki Kuu ya Tanzania, jijini Dar es Salaam.Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA), Bw. Nicodemas Mkama, akizungumnza katika hafla ya uzinduzi wa Kielelezo cha Viwango vya Faida vya Dhamana za Serikali (Government Securities Yield Curve), iliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Kilimanjaro, Benki Kuu ya Tanzania, jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mtendaji wa Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE), Bw. Peter Nalitolela, akizungumnza katika hafla ya uzinduzi wa Kielelezo cha Viwango vya Faida vya Dhamana za Serikali (Government Securities Yield Curve), iliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Kilimanjaro, Benki Kuu ya Tanzania, jijini Dar es Salaam.Baadhi ya washiriki wakifuatilia hotuba ya mgeni rasmi katika hafla ya uzinduzi wa Kielelezo cha Viwango vya Faida vya Dhamana za Serikali (Government Securities Yield Curve), iliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Kilimanjaro, Benki Kuu ya Tanzania, jijini Dar es Salaam.
Meza kuu ikiongozwa na Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Bw. Emmanuel Tutuba, (Katikati, walioketi), wakiwa katika picha ya pamoja na wadau baada ya kuzinduliwa rasmi kwa Kielelezo cha Viwango vya Faida vya Dhamana za Serikali (Government Securities Yield Curve), katika hafla iliyofanyika ukumbi wa mikutano wa Kilimanjaro, Benki Kuu ya Tanzania, jijini Dar es Salaam.
(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, WF, Dar es Salaam.)





































.jpeg)
.jpeg)




