Na Janeth Raphael – MichuziTv

Serikali imeeleza kuwa pamoja na mafanikio yanayoendelea kupatikana katika uhifadhi wa wanyamapori na maliasili, sekta hiyo bado inakabiliwa na changamoto mbalimbali zinazohitaji hatua endelevu, ikiwemo migongano kati ya binadamu na wanyamapori, ujangili, uvamizi wa maeneo ya hifadhi na shoroba pamoja na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Ashatu Kijaji (Mb), amesema hayo leo Septemba 11, 2026, wakati akizungumza katika hafla ya kufunga mafunzo kwa marubani wa ndege nyuki (drones) na kukabidhi vitendea kazi, iliyofanyika Mtumba, Dodoma.

Dkt. Kijaji amesema Serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali kuimarisha uhifadhi na usimamizi wa rasilimali za wanyamapori, lakini ongezeko la migongano kati ya binadamu na wanyamapori bado ni changamoto inayohitaji kupewa kipaumbele kutokana na madhara inayosababisha kwa wananchi, mifugo na mazao.

Amesema matukio hayo yanaweza pia kuathiri mtazamo wa jamii kuhusu uhifadhi wa wanyamapori, hivyo Serikali inaendelea kutafuta njia bora za kuzuia na kudhibiti migongano hiyo kabla haijasababisha madhara makubwa kwa wananchi.

Dkt. Kijaji amesema ujangili na biashara haramu ya nyara na mazao ya misitu ni miongoni mwa changamoto nyingine zinazoendelea kuhatarisha uwepo wa baadhi ya spishi za wanyamapori na uendelevu wa rasilimali za asili.

Amesema upanuzi wa shughuli za kibinadamu, ikiwemo kilimo, ufugaji, uchimbaji wa madini na ujenzi wa makazi katika maeneo yasiyozingatia mipango bora ya matumizi ya ardhi, umeongeza shinikizo katika maeneo ya hifadhi na kutishia kupotea kwa baadhi ya makazi muhimu ya wanyamapori.

Aidha, amesema uvamizi wa shoroba za wanyamapori umeendelea kuwa kikwazo kwa uhamaji wa wanyamapori kutoka eneo moja kwenda jingine, hali inayoweza kuathiri mifumo ya ikolojia inayounganisha maeneo mbalimbali ya hifadhi.

Dkt. Kijaji ametaja pia kuenea kwa mimea vamizi ndani ya maeneo ya hifadhi kuwa changamoto inayopunguza ubora wa makazi na malisho ya wanyamapori, huku mabadiliko ya tabianchi yakichangia ukame, mvua zisizotabirika, mafuriko, upungufu wa maji na uharibifu wa miundombinu ya uhifadhi.

Amesema katika kukabiliana na changamoto hizo, Serikali kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii imeendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ya kitaifa kwa kushirikiana na wananchi na wadau wa uhifadhi, huku ikiongeza matumizi ya teknolojia katika kuboresha usimamizi na ulinzi wa rasilimali hizo.

Dkt. Kijaji amesema katika mwaka wa fedha 2026/2027, Wizara imeweka kipaumbele katika kupunguza migongano ya binadamu na wanyamapori kupitia utekelezaji wa Mkakati wa Taifa wa Utatuzi wa Migongano ya Binadamu na Wanyamapori wa Miaka 10.

Amesema mkakati huo unalenga kuzuia, kudhibiti na kushughulikia kwa haraka matukio yanayohusisha wanyamapori wakali na waharibifu, ili kupunguza madhara kwa wananchi na kulinda usalama wa jamii.

Ametaja pia Mkakati wa Usimamizi na Uhifadhi wa Tembo wa Miaka 10, unaolenga kuimarisha uhifadhi endelevu wa tembo pamoja na kupunguza athari hasi dhidi ya wanyama hao na makazi yao.

Vilevile, Serikali inaendelea kutekeleza Mkakati wa Kuongoa na Kurasimisha Shoroba za Wanyamapori wa Miaka Mitano, unaolenga kuimarisha hali ya uhifadhi katika maeneo yanayotumiwa na wanyamapori wanapohama kutoka hifadhi moja kwenda nyingine au kutoka nchi moja kwenda nyingine ndani ya mifumo ikolojia inayovuka mipaka.

Amesema mfumo huo unasaidia mamlaka kupata taarifa kwa haraka na kuchukua hatua za kudhibiti matukio hayo, sambamba na kurahisisha mchakato wa ulipaji wa kifuta jasho au kifuta machozi kwa wananchi walioathirika.

Dkt. Kijaji amesema matumizi ya ndege nyuki (drones) nayo yanaendelea kupewa umuhimu katika ufuatiliaji na usimamizi wa maeneo ya uhifadhi, kwa lengo la kuongeza ufanisi katika ukusanyaji wa taarifa na kuwezesha hatua kuchukuliwa kwa wakati dhidi ya changamoto zinazojitokeza.

Amesisitiza kuwa mafanikio ya uhifadhi hayawezi kutegemea Serikali pekee, bali yanahitaji ushirikiano wa karibu kati ya Serikali, wananchi na wadau wa uhifadhi ili kuhakikisha rasilimali za wanyamapori zinalindwa, zinatunzwa na kunufaisha kizazi cha sasa na kijacho.






DENIS MLOWE, IRINGA


MKURUGENZI wa Bodi ya Maji Bonde la Rufiji, David Munkyala, amesema Serikali imeanza kuchukua hatua za kudumu katika kukabiliana na changamoto ya upatikanaji wa maji kwa mifugo na migogoro kati ya wakulima na wafugaji katika Tarafa ya Pawaga, Wilaya ya Iringa.

Munkyala amesema hayo wakati akizungumza na wanahabari juu ya hatua zilizochukuliwa na Bodi hiyo katika kuhakikisha wafugaji wanapata maji kwa ajili ya mifugo yao bila kulazimika kuingia katika maeneo ya mashamba au kutumia vyanzo vya maji vilivyopo kwenye maeneo ya miradi ya umwagiliaji.

Amesema changamoto hiyo ilijitokeza zaidi baada ya kuboreshwa kwa Skimu ya Umwagiliaji ya Mkombozi, ambapo awali wafugaji walikuwa wakipeleka mifugo kunywa maji katika maeneo ya mto na mabondeni, lakini baada ya maboresho ya skimu hiyo utaratibu huo ukabadilika na wafugaji kuzuiwa kupeleka mifugo katika maeneo ya mradi.

Munkyala alisema kuwa hali hiyo ilisababisha baadhi ya wafugaji kukosa maeneo mbadala ya kunyweshea mifugo na hivyo kuanza kuingia katika maeneo ya mashamba ya wakulima, jambo lililokuwa likichochea migogoro kati ya makundi hayo.

Amesema baada ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Kheri James, kutoa maelekezo mwezi Julai mwaka huu ya kutafutwa kwa njia mbadala ya kuwapatia wafugaji maji, Bodi ya Maji Bonde la Rufiji ilifanya utafiti na kuanza utekelezaji wa hatua hiyo kwa kuchimba kisima kirefu katika eneo hilo.

“Tumefanya survey na kuchimba kisima kirefu cha zaidi ya mita 100 na tumefanikiwa kupata maji ya kutosha. Kisima hiki kinatoa takribani lita 15 kwa sekunde, ambayo ni kiwango kikubwa cha maji,” amesema Munkyala.

Ameeleza kuwa lengo la kuchimba kisima hicho lilikuwa ni kuhakikisha wafugaji wanapata maji karibu na maeneo yao, hatua ambayo itasaidia kupunguza migogoro kati yao na wakulima, sambamba na kulinda vyanzo vya maji na mazingira.
Munkyala amesema matumizi ya mito na mabonde kwa ajili ya kunyweshea mifugo yanaweza kusababisha uharibifu wa kingo za mito, mmomonyoko wa udongo na kuongezeka kwa tope kwenye mito, hali ambayo inaweza kupunguza kina cha maji na kuathiri matumizi ya maji kwa shughuli mbalimbali, ikiwemo umwagiliaji na uzalishaji wa nishati.

“Kitendo cha mifugo kwenda mtoni kinaweza kuharibu kingo za mto na kusababisha mmomonyoko wa udongo na udongo huo huingia mtoni na kuongeza matope, jambo ambalo linaweza kupunguza kina cha mto na kuathiri matumizi ya maji kwa shughuli nyingine,” amesema.

Amesema ujio wa Mawaziri wawili wenye dhamana ya sekta ya kilimo pamoja na mifugo na uvuvi katika eneo hilo ni hatua muhimu kwa kuwa wamekuja kujionea utekelezaji wa mradi huo na kutafuta suluhisho la kudumu la changamoto zinazowakabili wakulima na wafugaji.

Munkyala, hatua zilizopendekezwa na Mawaziri hao zimeongeza matumaini ya kumaliza changamoto hiyo, baada ya kuahidi kuongeza miundombinu katika kisima kilichochimbwa pamoja na kuchimba visima vingine vitano kwa ajili ya kuwapatia wananchi na wafugaji maji.

Amesema kati ya visima hivyo, vitatu vinatarajiwa kuanza kuchimbwa kwa haraka na kuwezeshwa kwa miundombinu inayohitajika ili viweze kutumika na wananchi pamoja na wafugaji.

Amesema hatua hiyo itasaidia kupunguza utegemezi wa mifugo kwenda kwenye mabonde na mito kutafuta maji, hali ambayo imekuwa ikichangia migogoro na uharibifu wa mazingira.

Aidha, amesema Mawaziri hao wameelekeza Halmashauri kuhakikisha zinajenga miundombinu maalumu ya kunyweshea mifugo, huku zikitafutwa pia njia za kuongeza upatikanaji wa malisho kwa wafugaji.

Amesema miongoni mwa mikakati hiyo ni kuwezesha upandaji wa nyasi na kuboresha maeneo ya malisho ili mifugo ipate chakula cha kutosha na kupunguza ulazima wa wafugaji kupeleka mifugo katika maeneo ya mabondeni kwa ajili ya kutafuta maji na malisho.

Munkyala amewashukuru Mawaziri hao kwa kutembelea eneo la mradi na kutoa maelekezo yanayolenga kupata suluhisho la kudumu, akisema hatua hizo zitasaidia kuimarisha mahusiano kati ya wakulima na wafugaji, kulinda mazingira na kuhakikisha rasilimali za maji zinatumika kwa uendelevu.



Nyerere Cycling Tour Imetangaza washirika wa safari ya mwaka huu itakayokuwa na umbali wa kilomita 1,500 hadi Butiama, huku Vodacom Tanzania ikiendelea kuwa mshirika mkuu wa msafara huo, ikishirikiana na Afro Oil, Stanbic Bank Tanzania, BYD, ABC Bicycle, Coca-Cola na Huawei.

Akizungumza wakati wa mkutano na waandishi wa habari, Mkurugenzi wa uhusiano na Mawasiliano wa Vodacom Tanzania, Zuweina Farah, alisema Vodacom itaendelea kushirikiana na Nyerere Cycling Tour kama mshirika mkuu, akieleza kuwa ushirikiano huo unaonesha dhamira ya kampuni ya kuendelea kuunga mkono mipango yenye kuleta matokeo chanya kwa jamii nchini.

Alisema Vodacom pia inafurahia kuwapokea washirika wapya ambao ushiriki wao utaongeza thamani katika safari ya mwaka huu na kusaidia kupanua wigo na matokeo ya msafara huo.

Msafara huo utafanyika kuanzia tarehe 5 hadi 14 Oktoba 2026, ukiwa na mkazo katika elimu, afya na uhifadhi wa mazingira, sambamba na kuhamasisha wanafunzi, hususan wasichana, kushiriki katika michezo ya kuendesha baiskeli.

Katika safari ya mwaka huu, Vodacom wanatarajia kutoa madawati 1,000 kwa shule 10, kukarabati madarasa 40 na kujenga madarasa mapya 10, huku shughuli hizo zikitarajiwa kuwafikia zaidi ya wanafunzi 25,000. Katika safari zilizopita, Nyerere Cycling Tour ilifikia shule 107 na zaidi ya wanafunzi 75,000 walinufaika.

Akizungumzia ushirika wao, Meneja wa Uendelevu wa Stanbic Bank Tanzania, Annette Mkini, alisema benki hiyo itatumia msafara huo kuhamasisha elimu ya fedha kwa wanafunzi na vijana, ili kuwajengea uelewa itakayowasaidia kufanya maamuzi bora kuhusu matumizi na usimamizi wa fedha.

Kwa upande wake, Afro Oil imesema ushiriki wake unatokana na dhamira ya kampuni ya kurudisha kwa jamii, huku Samwel Msonsa kutoka BYD alisema kampuni hiyo itashiriki katika uzalishaji na uhamasishaji wa msafara huo, pamoja na shughuli za uhifadhi wa mazingira ikiwemo upandaji miti.

Msafara huo hadi sasa umesajili waendesha baiskeli 213, huku wengine wakitarajiwa kujiunga njiani. Waendesha baiskeli kutoka nchi 12 wanatarajiwa kushiriki, zikiwemo Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi, Malawi, Zambia, Afrika Kusini, Australia, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) na Uholanzi. Aidha, wanawake 23 tayari wamesajiliwa kushiriki katika msafara huo.

Vodacom pia ilitoa taarifa kuhusu Vodacom Coastal Classic, ambayo hadi sasa imeandikisha washiriki 147. Na washindi wa nafasi ya kwanza kwa wanawake na wanaume watapata Sh milioni 10 kila mmoja, nafasi ya pili Sh milioni 7 na nafasi ya tatu Sh milioni 5. Waendesha baiskeli watakaomaliza nafasi ya nne hadi ya kumi watapata Sh milioni 1 kila mmoja.

Vodacom Tanzania imewekeza Sh milioni 160 katika Msafara wa Baiskeli wa Nyerere, huku Vodacom Foundation ikichangia zaidi ya Sh milioni 300 kwa shughuli za kijamii zitakazotekelezwa katika maeneo yatakayopitiwa na msafara huo, ikiwemo uboreshaji wa shule na utoaji wa madawati. Safari hiyo itahitimishwa Butiama, nyumbani kwa Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.
Washirika wa Nyerere Cycling Tour, wakiongozwa na Mkurugenzi wa Uhusiano na Mawasiliano wa Vodacom Tanzania PLC, Zuweina Farah (wa nne kulia), ambaye aliwakilisha Vodacom Tanzania PLC kama mdhamini mkuu wa msafara huo, wakiwa katika picha ya pamoja wakati wa mkutano na waandishi wa habari na wadau wa msafara huo uliolenga kutangaza rasmi washirika wa zamani na wapya wa msafara huo. Katika picha kutoka kushoto ni Mkurugenzi wa Afroil, Mohamed Al-Jabry(wa pili kushoto) Meneja wa Uendelevu wa Stanbic Bank Tanzania, Annette Nkini (wa tatu kushoto), Mkuu wa Masoko na Mauzo wa BYD, Samwel Msonsa (wanne kushoto), Mwanzilishi wa Nyerere Cycling Tour, Gabriel Landa, Meneja wa Akaunti wa Vodacom Huawei, Victor Wang, na Katibu Mtendaji wa Coca-Cola Tanzania, Yvette Gadi. Mkutano huo ulifanyika jijini Dar es Salaam, Septemba 11, 2026
Baadhi ya washiriki wa msafara wa Nyerere cycling tour wakiwa katika mkutano na waandishi wa habari na wadau wa msafara huo uliolenga kutangaza rasmi washirika wa zamani na wapya wa msafara huo.

Mwanzilishi wa Nyerere Cycling Tour Gabriel Landa (wa kwanza kulia) akizungumza wakati wa mkutano na waandishi wa habari na washirika wao. Majadiliano hayo yalihusu namna gani watajumuika katika msafara huo.

Mwanzilishi wa Nyerere Cycling Tour Gabriel Landa akizungumza wakati wa mkutano na waandishi wa habari na wadau wa msafara. Mkutano huo ulilenga kutangaza rasmi washirika wa zamani na wapya wa msafara huo.
Washirika, Washiriki na Wadau wa Nyerere Cycling Tour wakiwa kwenye picha ya pamoja baada ya kuhitimisha mkutano wa waandishi wa habari uliopangwa kwa ajili ya kutangaza rasmi washirika wapya na wa zamani wa msafara huo.
Na Janeth Raphael - MichuziTv

Serikali imekabidhi ndege nyuki (drones) 40 kwa Taasisi za Uhifadhi za Tanzania (TANAPA), Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) na Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro (NCAA), ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kuongeza matumizi ya teknolojia katika kuimarisha ulinzi na uhifadhi wa rasilimali za wanyamapori nchini.

Ndege hizo zenye thamani ya takriban Shilingi bilioni 2.4 zimenunuliwa na Serikali kupitia Mfuko wa Uhifadhi wa Wanyamapori Tanzania (TWPF), kwa lengo la kuongeza uwezo wa doria za anga, kufuatilia mienendo ya wanyamapori wakali na waharibifu pamoja na kuwezesha upatikanaji wa taarifa kwa wakati halisi katika maeneo ya uhifadhi.

Akizungumza wakati wa hafla ya kufunga mafunzo ya marubani wa ndege nyuki na kukabidhi vitendea kazi kwa taasisi za uhifadhi na halmashauri jijini Dodoma, Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Ashatu Kijaji, amezitaka taasisi hizo kuhakikisha drones hizo zinasajiliwa na kupata vibali vyote vinavyohitajika kabla ya kuanza kutumika.

Dkt. Kijaji pia ameelekeza taasisi za uhifadhi kuwaandaa wataalam wa ndani kwa ajili ya matengenezo ya drones, hususan matengenezo madogo ambayo yanaweza kufanyika ndani ya uwezo wa taasisi, kutokana na changamoto ya upatikanaji wa wataalam wa matengenezo ya teknolojia hiyo katika maeneo mbalimbali.

Hatua hiyo inalenga kupunguza muda wa kusubiri huduma za matengenezo pindi ndege hizo zinapopata hitilafu na kuhakikisha zinaendelea kutumika kwa ufanisi katika shughuli za ulinzi na uhifadhi.

Mbali na drones, Serikali imekabidhi pikipiki 55 kwa Wakurugenzi wa Halmashauri za Wilaya, Miji na Jiji kwa ajili ya kuimarisha shughuli za udhibiti wa migongano kati ya binadamu na wanyamapori.

Kati ya pikipiki hizo, 40 zitatumiwa na Maafisa Wanyamapori wa Wilaya, huku pikipiki 15 zikitolewa kwa Jumuiya za Hifadhi za Wanyamapori za Jamii (WMA) saba, kwa lengo la kuongeza uwezo wa jamii kushiriki moja kwa moja katika shughuli za uhifadhi.

Kwa mujibu wa Waziri Kijaji, vitendea kazi hivyo vinatarajiwa kuongeza kasi na ufanisi wa operesheni za kudhibiti migongano kati ya binadamu na wanyamapori, hatua itakayosaidia kuokoa maisha ya wananchi, kulinda mali zao na kupunguza gharama za utekelezaji wa majukumu ya uhifadhi uwandani.

Amewataka Wakurugenzi wa Halmashauri na Maafisa Wanyamapori watakaopokea pikipiki hizo kuzitumia kwa malengo yaliyokusudiwa na kuzitunza ili ziweze kudumu na kutoa huduma kwa muda mrefu.

Katika hatua nyingine, Waziri Kijaji ameitaka TAWA kuimarisha usimamizi wa maeneo ya WMA na kuhakikisha mfumo huo unaleta manufaa ya moja kwa moja kwa jamii kupitia mapato yanayotokana na shughuli za utalii, huku ukisaidia kuimarisha ulinzi wa rasilimali za wanyamapori.

Amesema Serikali itaendelea kuweka mifumo ya kisheria na kiutendaji inayowezesha wananchi kushiriki katika uhifadhi, kwa kutambua kuwa ushiriki wa jamii ni sehemu muhimu ya kuhakikisha rasilimali za wanyamapori zinalindwa na kuleta manufaa kwa wananchi.

Aidha, amewataka Wakuu wa Taasisi za Uhifadhi kusimamia maadili ya watumishi na kuhakikisha vitendo vya ujangili, rushwa na uvunjifu wa sheria havipewi nafasi katika sekta ya uhifadhi.

Amesisitiza kuwa watumishi wanapaswa kutekeleza majukumu yao kwa uadilifu na kulinda heshima ya taaluma ya uhifadhi ili rasilimali za wanyamapori ziendelee kuwepo kwa manufaa ya kizazi cha sasa na vijavyo.

Katika hafla hiyo, Waziri Kijaji pia ametangaza kufungwa rasmi kwa mafunzo ya matumizi ya ndege nyuki yaliyowashirikisha marubani 52 kutoka TAWA, TANAPA, NCAA na Idara ya Wanyamapori (WD), huku akieleza matumaini kuwa mafunzo hayo yamewaongezea washiriki uwezo wa kiufundi na kitaalamu wa kutumia teknolojia hiyo katika kukabiliana na changamoto za wanyamapori wakali na waharibifu.

Amesema Serikali itaendelea kuwekeza katika teknolojia, rasilimali watu na mikakati shirikishi ili kuimarisha uhifadhi endelevu wa wanyamapori na kuhakikisha sekta hiyo inaendelea kuchangia maendeleo ya kijamii na kiuchumi nchini.

Kwa hatua hiyo, matumizi ya drones pamoja na kuongezeka kwa vitendea kazi kwa Maafisa Wanyamapori yanatarajiwa kuongeza uwezo wa Serikali na jamii katika kukabiliana na changamoto za uhifadhi, hususan migongano kati ya binadamu na wanyamapori, ujangili na ulinzi wa rasilimali za maliasili.







Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Deogratius Ndejembi, ameagiza Mamlaka na Taasisi zinazohusika kuchukua hatua za haraka kujiandaa ili kuzuia na kupunguza athari zinazoweza kusababishwa na mvua za El Niño zinazotarajiwa kuanza mwezi Oktoba 2026.

Makamu wa Rais ametoa maagizo hayo, mara baada ya kupokea taarifa ya utayari na maandalizi ya Serikali kufuatia tahadhari iliyotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania kuhusu mvua za El- nino, katika kikao kilichofanyika Ofisi ya Makamu wa Rais Jijini Dar es Salaam.

Akizungumza na Viongozi pamoja na timu ya wataalamu kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Wizara ya Ujenzi pamoja na Taasisi zilizochini ya Wizara hizo, Makamu wa Rais amesisitiza umuhimu wa taasisi zote zinazohusika, kufanya kazi kwa pamoja na kuchukua hatua za tahadhari mapema ili kuzuia au kupunguza athari zinazoweza kutokea kwa wananchi kufuatia ujio wa mvua hizo.

Pia amesisitiza umuhimu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama kushirikishwa katika maandalizi hayo ili kuwa na nguvu kazi ya kutosha pamoja na kuimarisha uwezo wa Serikali wa kuzuia, kupunguza na kukabiliana kwa haraka na athari zinazoweza kujitokeza.

“Ifanyike kampeni ya haraka, mikondo na mifereji ya maji izibuliwe, na barabara ziandaliwe,” amesisitiza Makamu wa Rais.

Aidha, ameelekeza taka, tope na udongo unaotolewa baada ya kuzibua mitaro na mifereji katika maeneo mbalimbali kuondolewa mara moja na kutupwa katika maeneo yaliyotengwa, badala ya kuachwa kandokando ya barabara ambako unaweza kurejea kwenye mifereji wakati mvua zinapoanza.

Makamu wa Rais pia ameagiza mamlaka husika kuwasimamia wakandarasi wanaotekeleza miradi ya ujenzi wa barabara, kuchukua hatua za haraka kusambaza vifusi vilivyorundikwa katika maeneo yenye shughuli za ujenzi, akisisitiza kuwa kazi hiyo haipaswi kusubiri hadi mvua zianze kunyesha kwani husababisha usumbufu na kero kwa wananchi.

Amesema katika maeneo yenye miradi ya ujenzi wa barabara ni lazima kuwe na mipango madhubuti itakayohakikisha barabara zinaendelea kupitika kwa urahisi na usalama, ili shughuli za ujenzi zisigeuke kuwa chanzo cha usumbufu au kuongeza athari kwa wananchi wakati wa mvua.

Katika kikao hicho, Makamu wa Rais alipokea taarifa kutoka kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, Mhe. Mhandisi Hamad Yusuf Masauni; Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Prof. Riziki Shemdoe; pamoja na Naibu Waziri wa Ujenzi, Mhandisi Godfrey Kasekenya.

Taarifa ziliyowasilishwa katika kikao hicho zimeeleza kuwa maandalizi yanaendelea vizuri kupitia Kamati ya Kitaifa iliyoundwa kuratibu hatua za kuzuia, kudhibiti na kukabiliana na majanga yanayoweza kujitokeza katika kipindi cha mvua za El Niño.

Miongoni mwa maeneo yaliyopewa kipaumbele ni kufanya tathmini ya makazi yaliyopo mabondeni na maeneo mengine yenye hatari ya mafuriko, kuongeza elimu na tahadhari kwa umma, kufanya tathmini ya masoko na maeneo yenye mikusanyiko mikubwa ya watu, pamoja na kuendesha kampeni za usafi wa mazingira.

Hatua nyingine ni kuzibua mitaro, mifereji na mikondo ya maji, kulinda njia za asili za maji, kudhibiti maji taka na kufanya ukaguzi wa madaraja pamoja na miundombinu mingine muhimu ili kubaini maeneo yenye hatari na kuchukua hatua kabla ya mvua kuanza.

Serikali pia imeweka mkazo katika kuwa na mpango shirikishi wa dharura utakaowezesha Taasisi mbalimbali kuratibu hatua za uokoaji na utoaji wa huduma muhimu endapo kutatokea mafuriko au majanga mengine yanayohusiana na mvua hizo.







Na. Peter Haule, WF, Nairobi, Kenya

Tanzania na Marekani zimeeleza dhamira ya kuendelea kuimarisha ushirikiano katika sekta mbalimbali za maendeleo, ikiwemo afya, kilimo, nishati, madini, miundombinu, elimu na utalii.

Dhamira hiyo imeelezwa wakati Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula (Mb), alipokutana na kufanya mazungumzo na Naibu Katibu wa Hazina ya Marekani anayeshughulikia Masuala ya Kimataifa, Bi. Erin Browne, mjini Nairobi, Kenya, kando ya Jukwaa la Mazungumzo ya Ngazi za Juu la Mawaziri wa Fedha kuhusu kuimarisha uwekezaji wa pamoja katika sekta ya afya.

Katika mazungumzo hayo, Mhe. Luswetula amezialika kampuni na wawekezaji kutoka Marekani kutumia fursa mbalimbali za uwekezaji zinazopatikana Tanzania, akitaja maeneo ya kilimo, nishati, madini, miundombinu, afya, elimu na utalii.

Aidha, Mhe. Luswetula ameishukuru Serikali ya Marekani kwa kuendelea kushirikiana na Tanzania pamoja na mchango wake katika maeneo mbalimbali ya maendeleo tangu kuanzishwa kwa uhusiano wa kidiplomasia kati ya nchi hizo mwaka 1968.

Amesema ushirikiano huo umekuwa na mchango katika juhudi za Tanzania za kukuza maendeleo ya kijamii na kiuchumi na kupunguza umaskini.

Kwa upande wake, Naibu Katibu wa Hazina ya Marekani anayeshughulikia Masuala ya Kimataifa, Bi. Erin Browne, amesema Marekani itaendelea kushirikiana na Tanzania katika maeneo mbalimbali ya maendeleo, pamoja na kuimarisha na kukuza ushirikiano uliopo baina ya nchi hizo.

Mazungumzo hayo yameangazia pia umuhimu wa kuendelea kujenga ushirikiano wa kiuchumi na uwekezaji kati ya Tanzania na Marekani kwa manufaa ya wananchi wa nchi hizo mbili.
Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula (Mb) akisalimiana na Naibu Katibu wa Hazina ya Marekani anayeshughulikia Masuala ya Kimataifa, Bi. Erin Browne, mjini Nairobi, Kenya, kando ya Jukwaa la Mazungumzo ya Ngazi za Juu la Mawaziri wa Fedha kuhusu kuimarisha uwekezaji wa pamoja katika sekta ya afya.



Naibu Katibu wa Hazina ya Marekani anayeshughulikia Masuala ya Kimataifa, Bi. Erin Browne, mjini Nairobi, Kenya, akizungumza kuhusu ushirikiano wa maendeleo wakati wa mkutano na Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula (Mb), kando ya Jukwaa la Mazungumzo ya Ngazi za Juu la Mawaziri wa Fedha kuhusu kuimarisha uwekezaji wa pamoja katika sekta ya afya.




Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula (Mb) (katikati), akieleza fursa za uwekezaji wakati wa mkutano na Naibu Katibu wa Hazina ya Marekani anayeshughulikia Masuala ya Kimataifa, Bi. Erin Browne kando ya Jukwaa la Mazungumzo ya Ngazi za Juu la Mawaziri wa Fedha Afrika, kuhusu kuimarisha uwekezaji wa pamoja katika sekta ya afya, wengine ni wajumbe walioambatana nae kutoka Tanzania.




Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula (Mb) (wa pili kushoto) na Naibu Katibu wa Hazina ya Marekani anayeshughulikia Masuala ya Kimataifa, Bi. Erin Browne (wa pili kulia) wakiwa katika mkutano kati yao, kando ya Jukwaa la Mazungumzo ya Ngazi za Juu la Mawaziri wa Fedha Afrika, kuhusu kuimarisha uwekezaji wa pamoja katika sekta ya afya.





Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula (Mb) na Naibu Katibu wa Hazina ya Marekani anayeshughulikia Masuala ya Kimataifa, Bi. Erin Browne wakiteta jambo, kando ya Jukwaa la Mazungumzo ya Ngazi za Juu la Mawaziri wa Fedha Afrika, kuhusu kuimarisha uwekezaji wa pamoja katika sekta ya afya.



(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Fedha)
Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Mheshimiwa Dkt. Rhimo Nyansaho (Mb), tarehe 10 Septemba 2026, amekutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Ulinzi na Uzalishaji wa Kijeshi na Amiri Jeshi Mkuu wa Jamhuri ya Kiarabu ya Misri, Mheshimiwa Luteni Jenerali Ashraf Salem Zaher, jijini El Alamein, Misri.

Mazungumzo hayo ya viongozi hao waandamizi yalilenga kujadili na kuimarisha maeneo mbalimbali ya ushirikiano baina ya Wizara za Ulinzi za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Jamhuri ya Kiarabu ya Misri, ambazo ni nchi rafiki zenye uhusiano wa muda mrefu na wa kihistoria.

Aidha, viongozi hao walijadili masuala mbalimbali ya kiulinzi na usalama, pamoja na utekelezaji wa mambo yaliyojadiliwa wakati wa ziara ya Rais wa Jamhuri ya Kiarabu ya Misri, Mheshimiwa Abdel Fattah el-Sisi, nchini Tanzania mnamo Julai 18, 2026, ambapo alifanya mazungumzo na mwenyeji wake, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Mazungumzo hayo yalisisitiza umuhimu wa kuendelea kuimarisha uhusiano na ushirikiano wa kiulinzi na kijeshi baina ya Tanzania na Misri, hususan katika maeneo yenye maslahi ya pamoja kwa manufaa ya mataifa hayo mawili.

Katika ziara yake nchini Misri, Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Mheshimiwa Dkt. Rhimo Nyansaho (Mb), pia alipata fursa ya kushiriki katika Maonesho ya Kimataifa ya Anga na Teknolojia za Anga za Juu ya El Alamein (EIAS), yanayofanyika jijini El Alamein, Misri.

Maonesho hayo yamewakutanisha viongozi waandamizi wa Serikali, Mawaziri wa Ulinzi, Wakuu wa Majeshi, viongozi wa mashirika na kampuni mbalimbali za kimataifa, wanazuoni pamoja na wataalamu kutoka sekta ya ulinzi na anga, kutoka zaidi ya nchi 60 duniani.

Ushiriki wa Tanzania katika maonesho hayo unaendelea kutoa fursa muhimu ya kubadilishana uzoefu, maarifa na teknolojia katika sekta ya ulinzi na anga, pamoja na kujenga na kuimarisha mahusiano ya kimkakati na wadau mbalimbali wa kimataifa katika maeneo yenye maslahi ya pamoja.







Na Jane Mwakyoma - Rukwa

MAMLAKA ya mawasiliano Tanzania (TCRA) imewakutanisha wadau mbalimbali mkoani Rukwa wakiwemo watoa huduma za mawasiliano ya simu, sekta ya usafiri, vyombo vya ulinzi na usalama pamoja na makundi mbalimbali ya kijamii, kwa lengo la kujadili namna ya kukabiliana na kutokomeza uhalifu wa mtandaoni unaoendelea kushika kasi mkoani humo.

Akifungua mkutano huo jana kwa niaba ya mkuu wa mkoa wa Rukwa mkuu wa wilaya ya Nkasi Peter Lijualikali amewataka wananchi kuendelea kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama kwa kutoa taarifa na kuripoti vitendo vya uhalifu wa mtandaoni, ikiwemo kuwabaini na kuwafichua wahalifu waliopo katika maeneo yao.

"Tushirikiane kwa pamoja katika kutokomeza uhalifu wa mitandaoni Rukwa bila matukio haya inawezekana nguvu ya pamoja inahitajika." Amesema Lijualikali.

kwa upande wake, mkurugenzi mkuu wa TCRA mhandisi Peter Mwasalyanda amesema bado kuna mwendelezo wa vitendo vya uhalifu vinavyofanyika kupitia huduma za simu na intaneti, huku mkoa wa Rukwa ukiendelea kukabiliwa na changamoto hiyo.

Amesema juhudi za kudhibiti vitendo hivyo zinahitaji ushirikiano wa karibu kati ya TCRA, vyombo vya ulinzi na usalama pamoja na jamii.

Akitoa takwimu mhandisi Mwasalyanda amesema mkoa wa Rukwa una jumla ya matukio 1330 kwa wilaya ya Sumbawanga, Kalambo 612, na wilaya ya Nkasi matukio 553.

Amesisitiza kuwa mafanikio katika kudhibiti uhalifu wa mtandaoni yanategemea ushirikiano wa wadau wote, kila mmoja akitimiza wajibu wake katika kuzuia na kupambana na vitendo hivyo.

Amesema TCRA itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali katika kutoa elimu na kuchukua hatua zinazolenga kuimarisha usalama wa watumiaji wa huduma za mawasiliano.

Aidha, wadau mbalimbali walioshiriki mkutano huo, wakiwemo viongozi wa dini, wamesisitiza umuhimu wa elimu, malezi bora na maadili mema katika jamii, hususan kwa watoto, ili kuwajengea uwezo wa kutambua na kujiepusha na vitendo vya uhalifu wa mtandaoni.

" Ni muhimu elimu ikatolewa kwa wananchi hasa waishio vijijini ili wawe na uelewa wa kutosha kwa kuwa wao ni wahanga wa matukio hayo " mmoja wa wadau amesema.









Kampuni ya mawasiliano ya Yas Tanzania imezindua minara miwili mipya ya 4G mkoani Kilimanjaro, ikiwa ni mwendelezo wa uwekezaji wake katika kupanua na kuboresha huduma za mawasiliano nchini.

Minara hiyo ambayo ipo katika wilaya ya Moshi Mjini na Mwanga inatarajiwa kuongeza uwezo na ubora wa mtandao, hususan huduma za intaneti, kwa wakazi, wafanyabiashara na taasisi katika maeneo hayo.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mkuu wa Yas - Kanda ya Kaskazini, Bw. Robert Sanyagi, alisema uwekezaji huo unatokana na ongezeko la mahitaji ya huduma za mawasiliano na matumizi ya huduma za kidijitali.

“Leo Watanzania wanahitaji zaidi ya huduma za kupiga simu. Wanahitaji intaneti yenye kasi na uhakika kwa ajili ya biashara, elimu, huduma za kifedha na shughuli nyingine za kila siku. Ndiyo maana tunaendelea kuwekeza katika teknolojia za 4G na 5G ili kuwafikia wananchi wengi zaidi,” alisema Sanyagi.

Alisema Yas itaendelea kupanua mtandao wake katika maeneo mbalimbali nchini, ikiwemo maeneo ya mijini na pembezoni, ili wananchi wanufaike na fursa zinazotokana na ukuaji wa uchumi wa kidijitali.

Akizindua mnara huo, mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Moshi ambaye ni Afisa Tarafa wa Moshi Mashariki, Bi. Khalima Idrisa, amesema mnara huo utaimarisha mawasiliano na kusaidia juhudi za Serikali katika kuboresha huduma hizo kwa wananchi.

Kwa upande wake, mkazi wa Kilimanjaro, Bi. Mwanaisha Juma, aliishukuru Yas na kusema kuwa kuimarika kwa huduma za mawasiliano kutapunguza changamoto ambazo wananchi walikuwa wakikumbana nazo hapo awali.

“Zamani tulikuwa tunapata changamoto kubwa sana za kimawasiliano, hasa kwenye huduma za kutuma na kupokea fedha. Wakati mwingine fedha zilikuwa zinachelewa kufika. Lakini sasa hivi hali imebadilika; huduma nyingi zinapatikana kwa urahisi kupitia mtandao. Tunaamini maboresho haya yataturahisishia zaidi maisha na shughuli zetu za kila siku,” alisema Bi.Mwanaisha.

Yas Tanzania imesema uzinduzi wa minara hiyo ni sehemu ya uwekezaji unaoendelea katika Kanda ya Kaskazini na maeneo mengine nchini, kwa lengo la kuwafikishia Watanzania huduma za mawasiliano zenye kasi na uhakika.




MAHAKAMA Kuu ya Tanzania imeamuru kutolewa kwa wito (summons) kwa Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP), Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi (CDF) na Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai (DCI), ili kutoa ushahidi katika kesi ya uhaini inayomkabili Mwenyekiti wa CHADEMA, Tundu Lissu.

Uamuzi huo umetolewa leo na jopo la majaji watatu wakiongozwa na Jaji Dustan Ndunguru baada ya Mahakama kusikiliza hoja za upande wa mashtaka na utetezi kuhusu ombi la Lissu la kuwaita mashahidi hao pamoja na viongozi wengine wa Serikali.

Mahakama imesema, kwa kuzingatia kifungu cha 314 cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai (CPA), ina hiari ya kuruhusu mashahidi kuitwa kwa kuangalia umuhimu wa ushahidi wao katika shauri.

Katika uamuzi huo, Mahakama imesema imeridhika kuwa ushahidi wa IGP, CDF na DCI ni muhimu katika kesi hiyo, hivyo imeamuru summons zitolewe ili waje kutoa ushahidi upande wa utetezi.

Hata hivyo, Mahakama imekataa ombi la kuwaita baadhi ya mashahidi waliotajwa na Lissu, akiwemo Rais Samia Suluhu Hassan na Waziri Mkuu wa zamani Kassim Majaliwa, ikisema ushahidi wao hauhusiani na kesi hiyo kwa upande wa utetezi.

Mahakama pia imekubaliana na hoja ya upande wa mashtaka kwamba mashahidi ambao hawakutajwa wakati wa committal proceedings hawawezi kutajwa baadaye wakati wa usikilizwaji wa hoja za awali (PH).

Jaji Ndunguru amesema kifungu cha 281 cha CPA kinaeleza kuwa msajili atatoa summons kwa mashahidi waliotajwa wakati wa committal proceedings, huku Mahakama ikibaini kuwa katika mwenendo wa kesi hiyo hakukuwa na orodha ya mashahidi waliotajwa.

Kuhusu hoja ya kumuita Mkurugenzi wa Usalama wa Taifa, Mahakama imesema mfano wa kesi ya Khatibu Ghandi hauwezi kutumika moja kwa moja kwa kuwa katika kesi hiyo shahidi huyo aliitwa na upande wa mashtaka na pia sheria ya sasa ya Usalama wa Taifa haikuwepo wakati huo.

Kesi hiyo imeahirishwa hadi kesho saa tatu asubuhi kwa ajili ya kuendelea na hatua ya utetezi.


Wadau wa kilimo-misitu nchini Tanzania wameanzisha jukwaa maalum (TASP), litakalowaunganisha wadau mbalimbali kwa ajili ya kubadilishana uzoefu, taarifa na ubunifu, pamoja na kuimarisha ushirikiano katika kuendeleza kilimo-misitu na kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi.

Akifungua jukwaa hilo Septemba 10, 2026 jijini Dodoma, Afisa Mazingira kutoka Wizara ya Kilimo, Nickson Kimaro, amesema kilimo-misitu ni agenda mtambuka inayohitaji ushirikiano wa Serikali, wakulima, taasisi za utafiti, sekta binafsi, asasi za kiraia, taasisi za fedha na washirika wa maendeleo.

Amesema TASP inapaswa kuwa mfumo endelevu wa uratibu utakaowezesha wadau kuoanisha jitihada zao, kubaini mapungufu na kutumia rasilimali kwa ufanisi, huku kilimo-misitu kikiwa na manufaa ya kiuchumi, kijamii na kimazingira.

Mkurugenzi Mtendaji wa Civic Social Protection Foundation (CPS), Nemence Iriya, amesema jukwaa hilo litatoa nafasi kwa wadau kukutana na kujadili sera, mikakati, sheria na taratibu zinazohusu kilimo-misitu, pamoja na kuimarisha uratibu wa shughuli zao.

Amesema TASP pia itasaidia kuhakikisha matokeo ya tafiti na ubunifu unaofanywa na watafiti unawafikia wakulima moja kwa moja, pamoja na watunga sera na wafanya maamuzi, na kuhalikisha tafiti hizo zinatumika katika kuboresha mipango na mikakati ya kilimo-misitu.

Kwa upande wake, Afisa Utafutaji Rasilimali Fedha, Mawasiliano na Utetezi kutoka VI-Agroforestry, Khalid Ngassa, amesema jukwaa hilo litawawezesha wadau kukutana pamoja, kubadilishana maarifa na uzoefu na kujadili changamoto zinazowakabili ili kupata suluhisho kwa pamoja.

Kwa ujumla, kuanzishwa kwa jukwaa hilo, kunatoa fursa muhimu ya kuwaunganisha wadau wa kilimo-misitu na kujenga mshikamano katika kushughulikia changamoto zinazowakabili, huku mafanikio ya jukwaa hilo yakitegemea utekelezaji wa mijadala na maazimio yaliyowekwa ili kuleta matokeo yanayoonekana kwa wakulima, kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi pamoja na maendeleo ya sekta hiyo nchini.














Na Nasra Ismail, Geita

Shirika la Arusha Society for the Protection of Animals (ASPA) kwa kushirikiana na Brooke East Africa limeendelea kutoa elimu kwa wafugaji na waendesha punda katika Kata ya Magenge, Halmashauri ya Wilaya ya Geita. Hii imechangia kuboresha ustawi wa mnyama kazi huyo katika maeneo hayo.

Kupitia elimu wanayopatiwa na mashirika hayo, wamiliki na waendesha punda wameanza kuona faida ya kumtunza mnyama huyo ambaye sasa ameanza kuwaingizia kipato tofauti na awali.

Wananchi wamesema sasa wana elimu ya kumtunza punda na namna sahihi ya kumfungia mkokoteni. Hii imesaidia kumpunguzia mnyama huyo vidonda na mateso, tofauti na kipindi kilichopita kabla ya kupata elimu hiyo.

Afisa Mifugo wa Kata ya Magenge, George Sebastianamesema kupitia elimu inayotolewa na ASPA, kwa kipindi kirefu sasa punda wameanza kuzaliana. Hii inaonesha kuwa punda sasa wanapata ustawi na wanaishi vizuri.

Kwa upande wake, Afisa Elimu ya Ustawi wa Wanyama kutoka ASPA, Diana Msemo amesema mnyama kazi punda anahitaji utulivu wa hali ya juu ili aweze kufanya kazi zake za kiasili na kuongeza uwezekano wa kupata ujauzito na kuongeza kizazi chake.

Msemo amebainisha baadhi ya mambo yanayompa utulivu mnyama huyo ni pamoja na kupata muda wa kupumzika, kupewa matibabu ya mara kwa mara na kupunguziwa mizigo ambayo haimudu.

 





Top News