Na Belinda Joseph.

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Ukaguzi na Usimamizi wa Vyama vya Ushirika Tanzania (COASCO), CPA Jeremia Jackson Mugeta, amesema shirika hilo limepokea na liko tayari kutekeleza maagizo yaliyotolewa na Makamu wa Rais, Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, ya kuhakikisha linavikagua na kuvisimamia vyama vya ushirika pamoja na kuwasilisha taarifa kuhusu hali ya ushirika nchini.

CPA Mugeta amesema hayo alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya maadhimisho ya Siku ya Ushirika yaliyofanyika katika Kijiji cha Ushirika ndani ya viwanja vya Maonesho ya Nanenane kitaifa jijini Dodoma Agosti 3, 2026.

Ameeleza kuwa katika mwaka wa fedha 2026/2027 shirika hilo lilianza maandalizi ya ukaguzi kuanzia Julai 20 kwa kuandaa mpango kazi, huku wataalamu wakiendelea kuratibu zoezi hilo ambalo litahusisha vyama vyote vya ushirika vilivyofunga hesabu zake Machi 31, 2026.

Amefafanua kuwa kwa mujibu wa sheria, vyama vya ushirika vinapofunga hesabu zake hupewa miezi mitatu kuandaa na kuwasilisha taarifa za fedha kwa mkaguzi wa nje ambaye ni COASCO, na kwamba mara baada ya maonesho ya Nanenane wakaguzi wataanza kwenda katika maeneo ya vyama hivyo kwa ajili ya kufanya ukaguzi.

CPA Mugeta amesema COASCO itatekeleza maagizo yote yaliyotolewa na Makamu wa Rais na kuwasilisha taarifa kwa mamlaka husika kulingana na ratiba ya kisheria, ambapo ripoti ya kwanza itawasilishwa mwezi Januari 2027 kwa Waziri wa Kilimo baada ya kukamilika kwa kipindi cha miezi sita.

Amesema katika mwaka wa fedha uliopita COASCO ilikuwa na lengo la kukagua takribani vyama 5,000 vya ushirika, ambapo ilifanikiwa kukagua vyama 4,858, huku lengo la mwaka wa fedha 2026/2027 likiwa ni kukagua vyama vyote vya ushirika nchini.

Aidha, ametoa wito kwa vyama vya ushirika kuzingatia sheria kwa kufunga hesabu zao kwa wakati na kuziwasilisha kwa COASCO kwa ajili ya ukaguzi.

Amesisitiza kuwa mafanikio ya zoezi hilo yanategemea ushirikiano wa kila chama cha ushirika kutekeleza wajibu wake kwa mujibu wa sheria, akionya kuwa vyama vitakavyokiuka taratibu na sheria vitachukuliwa hatua na Mrajis wa Vyama vya Ushirika.



 Na: Mwandishi wetu - Dodoma

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Mwigulu Lameck Nchemba ameipongeza Mamlaka ya Afya ya Mimea na Viatilifu Tanzania (TPHPA) kwa kazi nzuri ya kuhifadhi mbegu za asili na kupambana na wadudu na magonjwa ya mimea na hivyo kuchangia utoshelevu wa chakula na kuongeza mapato.

Mkurugenzi Mkuu wa TPHPA Prof. Joseph Ndunguru akitoa maelezo kwa waziri Mkuu wakati alipotembelea banda hilo kwenye maonesho wa wakulima Nanenane Jijini Dodoma.

Pongezi hizo amezitoa wakati alipotembelea banda TPHPA kabla ya kufungua rasmi maonesho ya wakulima Nanenane kitaifa Jijini Dodoma na kuelezwa kazi mbalimbali ambazo zinatekelezwa na mamlaka hiyo zinazoleta tija kwenye maendeleo ya sekta ya kilimo na biashara ya uuzaji mazao nje ya nchi.

“Nawapongeza kwa kazi nzuri mnayoifanya katika kusaidia kutimiza malengo ya Serikali hasa katika eneo la sekta ya kilimo ambayo inaajiri Watanzania wengi kuliko sekta nyingine yoyote, endeeeni kuchapa kazi nasi kwa upande wetu kama Serikali tutaendelea kuwaunga mkono katika kuboresha mazingira ya kazi zenu kwa kuwapatia vifaa na mahitaji mengine muhimu ili kuongeza tija” alisema Mhe. Nchemba.

Awali akitoa maelezo ya kazi za Mamlaka hiyo kwa Waziri Mkuu, Mkurugenzi Mkuu wa TPHPA Prof. Joseph Ndunguru amesema pamoja na majukumu mengi waliyonayo lakini wanasaida kuhakikisha mazao yanayozalishwa na wakulima nchini yanapimwa ubora wake na kufikia viwango vinavyohitaji kwenye masoko mbalimbali duniani na hivyo kuingizia taifa fedha za kigeni.

“Ili makampuni mbalimbali kutoka Tanzania yaweze kuuza mazao kwenye masoko mbalimbali nje ya nchi kuna vigezo ambavyo masoko hayo yanahitaji kwenye mazao hayo, hivyo sisi kama mamlaka tunasaidia kuhakikisha makampuni hayo yanapata bidhaa zenye kukidhi viwango hivyo na hivyo kuwezesha kufikia soko kulingana na mahitaji ya kila soko na bidhaa inapouzwa” alieleza Prof. Ndunguru.

Prof. Ndunguru amesema pia jukumu hilo linakwenda sambamba na kudhibiti visumbufu vya mazao ikiwemo Magonjwa na wadudu waharibifu wa mazao ili wakulima waweze kulima kilimo chenya tija na kazi hiyo inafanywa kwa kutumia teknolojia za kisasa kabisa za utambuzi na udhibiti ikiwemo kipimo cha Vinasaba (DNA) ambacho kinauwezo wa kupima kinasaba cha kiumbe chochote  na kutoa majibu ndani ya dakika 20.

“Teknolojia hii ya kisasa tunaenda nayo mahali popote huko kwenye mshamba ya wakulima, tunachukua sampuli na kupima hapohapo shambani mkulima akiona na ndani ya dakika 20 tunapata majibu kuwa ni Kirusi gani, Bakteria gani au Fangasi yupi na kupendekeza kiuatilifu gani au mbinu gani sahihi inafaa kutumika kutatua changamoto iliyoonekana” alifafanua Mkurugenzi huyo Mkuu wa TPHPA Prof. Ndunguru.

Aidha amesema kuwa kazi nyingine ambayo TPHPA inafanya ni kutunza nasaba za mimea kwa maana ya Mbegu za asili zote na mpaka sasa benki hiyo ya mbegu ina aina elfu kumi (10,000) zimetuzwa  kutoka mikoa mbalimbali na za mazao aina mbalimbali zile za asili kabisa zinazotambuliwa na jamii na zingine zilikuwa zinaelekea kupotea lakini wamefanikiwa kuzitunza.

Pia Prof. Ndunguru amesema jukumu lingine muhimu la mamlaka hiyo ni kutoa mafunzo ya matumizi salama ya Viuatilifu pamoja na kuangalia ubora wa Viuatilifu vilivyopo na vile vinavyoingia nchini kwa kutumia mitambo na vifaa vya kisasa vilivyopo makao makuu ya TPHPA pale Arusha na kwenye ofisi za kanda ya mamlaka hiyo ili kusaidia wakulima kupata viuatilifu salama na kuvitumia kwa usahihi bila kuleta adhari kwao, mazao na mazingira.

“Kupitia jukumu hilo Mamlaka imeiongezea Serikali mapato katika mizigo ambayo inasafirishwa kutoka nchini kwenda nje ya nchi lakini pia kufanikiwa kufungua masoko mbalimbali ya bidhaa ambayo nchi yetu ilifungiwa kutokana na kutokidhi mahitaji ya masoko yao na sasa watanzania na makampuni yanauza mazao yetu kwa wingi kwenye masoko hayo “alifafanua Prof. Ndunguru.

Mamlaka ya Afya ya mimea na Viuatilifu Tanzania TPHPA inashiriki kwenye maonesho ya wakulima Nanenane kwenye kanda zote ikiwemo Pwani, Kanda ya kati Dodoma, Kanda ya Kaskazini jijini Arusha, Kanda ya Kusiki Mbeya na Kanda ya Magharibi Simiyu.


MATUKIO KATIKA PICHA WAZIRI MKUU ALIPOTEMBEA BANDA LA TPHPA KWENYE MAONESHO HAYO.









 

 

 

 

 

 Na: Calvin Gwabara – Dodoma.

Mamlaka ya Afya ya Mimea na Viuatilifu Tanzania (TPHPA) imeeleza kuwa imefanikiwa kuokoa zaidi ya tani milioni 2.1 za chakula msimu uliopita na ekari zaidi ya 700,000 baada ya kudhibiti milipuko ya visumbufu vya mazao, ikiwemo ndege aina ya Kwelea kwelea, Panya na Viwavi Jeshi.

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. James Kinyasi Millya (Kulia) akimsikiliza Mkurugenzi Mkuu wa TPHPA Prof. Joseph Ndunguru

Akizungumza jijini Dodoma kwenye maonesho ya wakulim Nanenane kitaifa, Mkurugenzi Mkuu wa TPHPA, Prof. Joseph Ndunguru, amesema mamlaka hiyo ina mchango mkubwa katika kuhakikisha Tanzania inafikia utoshelevu wa chakula unaofikia asilimia 130, kupitia udhibiti wa wadudu, magonjwa ya mimea na visumbufu mbalimbali vinavyohatarisha uzalishaji wa mazao.

Amesema katika msimu uliopita, TPHPA ilidhibiti uvamizi wa ndege aina ya kwelea kwelea wapatao milioni 231 waliovamia skimu kubwa za mpunga, hususan maeneo ya Mbarali Mkoani Mbeya, Bariadi Mkoani Simiyu na Kilosa Mkoani Morogoro, hatua iliyosaidia kuokoa zaidi ya tani milioni 1.6 za chakula.

“Kwa mfano, tunadhibiti visumbufu milipuko kama vile ndege aina ya Quelea quelea, ambao wanaharibu nafaka kwa kula mpunga, mtama na uwele. Msimu uliopita tulikuwa na uvamizi wa ndege hao wapatao milioni 231 katika skimu kubwa za mpunga. Tulienda kuwazuia kwa kutumia ndege maalum na tuliweza kuokoa zaidi ya tani milioni 1.6 za chakula,” amesema Prof. Ndunguru.

Aidha, amesema mamlaka hiyo ilidhibiti uvamizi wa panya katika mikoa 19 na wilaya 54, ambapo hatua zilizochukuliwa ziliwezesha kuokoa takribani ekari 408,000 za mazao huku kwa upande wa viwavi jeshi vamizi waliokoa zaidi ya ekari 219,000, ambapo udhibiti wake uliwezesha kuokoa tani 519,000 za mahindi.

Amesema jitihada hizo zimechangia kuongeza uzalishaji wa mahindi nchini na kuipandisha Tanzania kutoka nafasi ya tatu hadi ya pili kwa uzalishaji wa mahindi barani Afrika, ikitanguliwa na Afrika Kusini.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. James Kinyasi Millya, ameipongeza TPHPA kwa juhudi zake za kuhakikisha wakulima wanapata masoko ya uhakika kwa mazao yao kwani uzalishaji mkubwa bila soko kunaweza kuwakatisha tamaa wakulima.

Amesema Serikali kupitia Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki iko tayari kushirikiana na TPHPA katika kutafuta masoko ya mazao ya Tanzania kupitia balozi za nchi hiyo zilizopo katika mataifa mbalimbali duniani.

“Jambo kubwa ambalo nimelifurahia ni jinsi mnavyopambana kutafuta masoko ya wakulima wetu. Tunahimiza kuzalisha sana, lakini mwisho wakikosa masoko na kupata hasara wanaweza kukata tamaa. Hivyo, nyinyi mnatusaidia sana kwa upande wa Serikali kuondoa changamoto hiyo,” amesema Mhe. Millya.

Amesema ushirikiano huo ni sehemu ya maagizo maalumu ya Rais kwa mabalozi wa Tanzania kushirikiana na taasisi zinazohusika na uzalishaji na biashara ya mazao ili kuwezesha bidhaa za wakulima wa Tanzania kupata masoko katika nchi wanazowakilisha.

Mhe. Millya ameitaka TPHPA kutumia fursa zilizopo katika masoko ya kimataifa, akitolea mfano zao la ndizi zinazozalishwa Bukoba na kupelekwa katika baadhi ya masoko ya nje, ikiwemo Marekani na Canada.

“Naomba TPHPA iangalie fursa ya zao la ndizi za Bukoba zinazokwenda Marekani, Canada na nchi nyingine, shirikianeni na balozi zetu kuona namna gani tunaweza kupeleka ndizi zetu katika nchi hizo na kuongeza masoko kwa wakulima wetu,” amesema Mhe. Millya.

Amesema ushirikiano kati ya TPHPA na Wizara ya Mambo ya Nje ni muhimu katika kuhakikisha mazao ya Tanzania yanapata masoko ya uhakika nje ya nchi, huku akisisitiza kuwa Serikali itaendelea kuweka mazingira wezeshi kwa wakulima na wadau wa sekta ya kilimo kuongeza uzalishaji na tija. 


MATUKIO KATIKA PICHA KWENYE BANDA LA TPHPA 





Na Janeth Raphael - MichuziTv 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema kuwa kulinda amani na utulivu wa nchi ni hatua muhimu ya kuhakikisha uwekezaji unaendelea kukua, ajira zinapatikana na uchumi unaimarika.

Akizungumza katika Mkutano Maalum wa Serikali na Sekta Binafsi kuhusu utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 uliofanyika Ikulu, Dar es Salaam, Rais Samia alisema maendeleo hayawezi kupatikana bila mazingira salama yanayowapa wawekezaji na wafanyabiashara uhakika wa kufanya shughuli zao.

Ameitaka sekta binafsi kuongeza uwekezaji, uzalishaji, matumizi ya teknolojia na ubunifu, huku ikiwapa nafasi vijana, wanawake na watu wenye ulemavu kushiriki kikamilifu katika shughuli za uzalishaji na mnyororo wa thamani. Pia amesisitiza umuhimu wa kuongeza thamani ya mazao, kuzingatia viwango vya ubora na kupanua biashara katika masoko ya Afrika na duniani.

Katika mkutano huo, Rais Samia alizindua nyenzo za utekelezaji wa Dira 2050 na kukabidhi Ufunguo wa Mtazamo Mpya unaoashiria mwanzo wa ushirikiano mpya kati ya Serikali na sekta binafsi. Aidha, aliiagiza Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji kuhakikisha wadau wote wanafahamu nyenzo hizo ili kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wa dira hiyo.

Kwa upande wake, Rais wa Zanzibar, Dkt. Hussein Ali Mwinyi, aliahidi ushirikiano wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kutekeleza Dira 2050, akieleza kuwa maeneo ya uwekezaji, sayansi, teknolojia, uchumi wa kidijitali, uchumi wa buluu na maendeleo ya rasilimali watu yatapewa kipaumbele.

Naye Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, Prof. Kitila Mkumbo, alisema maboresho ya mazingira ya biashara yameongeza imani ya wawekezaji na kuifanya Tanzania kuvutia zaidi mitaji, huku Rais wa Shirikisho la Sekta Binafsi Tanzania (TPSF), Angelina Ngalula, akipongeza hatua zilizochukuliwa na Serikali katika kuboresha sera, sheria na mifumo ya uwekezaji.

Wawakilishi wa sekta binafsi waliihakikishia Serikali kuendelea kushirikiana katika kuongeza uwekezaji, teknolojia na ajira, huku wakisisitiza umuhimu wa sera zinazotabirika na mashauriano ya mara kwa mara kuhusu mazingira ya biashara.

Katika hafla hiyo, Rais Samia pia alishuhudia utiaji saini wa Tamko la Pamoja kati ya Serikali na Sekta Binafsi kuhusu utekelezaji wa Dira 2050, kabla ya kutunukiwa Tuzo ya Heshima kutoka sekta binafsi kwa mchango wake katika kuboresha mazingira ya biashara, uwekezaji na kukuza uchumi shirikishi nchini.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea Tuzo ya Heshima kutoka Rais wa Chemba ya Taifa ya Biashara Tanzania (TNCC), Bw. Vicent Minja katika hafla ya uzinduzi wa Nyenzo za Utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 03 Agosti, 2026.




Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na viongozi mbalimbali kabla ya kuzindua Nyenzo za Utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 03 Agosti, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwakabidhi mfano wa Ufunguo kama ishara ya mtazamo mpya, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji Profesa Kitila Mkumbo, Waziri wa Fedha na Mipango Zanzibar, Dkt. Juma Malick Akil, Rais wa Shirikisho la Sekta Binafsi Tanzania (TPSF) Bi. Angelina Ngalula pamoja na Mwenyekiti wa Chemba ya Biashara Zanzibar (ZNCC), Bw. Ali Amour baada ya uzinduzi Nyenzo za Utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 03 Agosti, 2026.

Na Janeth Raphael - MichuziTv

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Emmanuel Nchimbi, ameielekeza Tume ya Maendeleo ya Ushirika kuimarisha ukaguzi wa mara kwa mara katika vyama vya ushirika nchini ili kudhibiti ubadhirifu wa mali, kuongeza uwajibikaji na kuhakikisha vyama hivyo vinatoa huduma bora kwa wanachama wake.

Dkt. Nchimbi amesema Serikali imejipanga kuifanya sekta ya ushirika kuwa nguzo muhimu ya maendeleo ya kilimo na uchumi wa taifa kwa kuhakikisha mali za vyama vya ushirika zinalindwa, zinasimamiwa kwa ufanisi na zinatumika kwa manufaa ya wakulima na wanachama wote.

Amesema ukaguzi wa mara kwa mara utasaidia kubaini mapema changamoto zinazojitokeza katika vyama vya ushirika, hivyo kuwezesha hatua stahiki kuchukuliwa kabla ya kusababisha hasara au matumizi yasiyo sahihi ya rasilimali za wanachama.

Aidha, Dkt. Nchimbi amesisitiza kuwa Serikali itaendelea kuweka mazingira rafiki yatakayowezesha vyama vya ushirika kuimarika zaidi ili viweze kuongeza mchango wake katika kuinua uzalishaji wa kilimo, kuongeza kipato cha wakulima na kuchochea ukuaji wa uchumi wa Taifa.

Ameeleza kuwa kwa sasa Tanzania ina vyama vya ushirika 2,531 ambavyo vinaendelea kuwa daraja muhimu la kuwafikishia wananchi huduma mbalimbali, hususan katika sekta ya kilimo, na kusisitiza kuwa vinapaswa kuendelea kuimarishwa ili viendane na mahitaji ya maendeleo ya nchi.

"Vyama vya ushirika vina nafasi kubwa katika maendeleo ya wananchi. Tunapaswa kuviwezesha na kuviimarisha ili viweze kutoa huduma bora zaidi na kuchochea maendeleo ya kiuchumi," amesema Dkt. Nchimbi.

Pia amepongeza mafanikio yaliyopatikana katika sekta hiyo, akibainisha kuwa thamani ya biashara iliyofanywa kupitia vyama vya ushirika imeongezeka kutoka Sh trilioni 4.2 hadi kufikia Sh trilioni 4.9 katika msimu wa mwaka 2025/2026.

Ameongeza kuwa upatikanaji wa mitaji ni msingi muhimu wa kuimarisha uwekezaji katika sekta ya kilimo, hivyo Serikali itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kuhakikisha wakulima wanapata fursa za kifedha zitakazowawezesha kuongeza uzalishaji na thamani ya mazao yao.

Kwa upande wake, Mrajisi wa Vyama vya Ushirika, Benson Ndiege, amesema Tume ya Maendeleo ya Ushirika imeanzisha mfumo maalumu wa kutambua na kuhakiki mali zinazomilikiwa na vyama vya ushirika nchini kwa lengo la kuwa na taarifa sahihi zitakazorahisisha usimamizi na matumizi yake.

Amesema mfumo huo utawezesha kujua thamani halisi ya mali za vyama vya ushirika, kuboresha utoaji wa huduma kwa wanachama na kuongeza uwazi katika usimamizi wa rasilimali za vyama hivyo.

Ndiege amesema hadi sasa mali 5,558 za vyama vya ushirika zimetambuliwa na kufanyiwa tathmini, zikiwa na thamani ya Sh milioni 18.6, huku akisisitiza kuwa zoezi hilo litaendelea sambamba na ukaguzi wa mara kwa mara ili kuhakikisha sheria, kanuni na taratibu za ushirika zinafuatwa.

Aidha, ametoa wito kwa wanachama na wadau wa sekta ya ushirika kushirikiana na Tume kwa kutoa taarifa na ushirikiano utakaosaidia kulinda mali za vyama hivyo na kuimarisha utendaji wake.

Naye Waziri wa Kilimo, Godfrey Chongolo, amesema Serikali itaendelea kuifanya sekta ya ushirika kuwa sehemu muhimu ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kwa kuhakikisha vyama vya ushirika vinaendeshwa kwa misingi ya uwazi, ufanisi na uwajibikaji.

Amesema Wizara ya Kilimo itaendelea kuhamasisha wananchi kujiunga na vyama vya ushirika vinavyofanya kazi kwa kuzingatia sheria, huku ikichukua hatua kali za kisheria dhidi ya wote watakaobainika kukiuka misingi na taratibu za ushirika.







Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, amesema Kijiji cha Ushirika kilichoandaliwa katika Maonesho ya Kilimo ya Nanenane Kitaifa jijini Dodoma kimeonesha kwa vitendo mchango mkubwa  wa ushirika katika kukuza uchumi wa wakulima kupitia uzalishaji, masoko, huduma za kifedha na uongezaji thamani wa mazao.

Akizungumza katika Siku ya Ushirika iliyofanyika ndani ya Kijiji cha Ushirika kwenye maonesho hayo Agosti 8, 2026, amesema kijiji hicho si eneo la maonesho pekee, bali ni sehemu ya kuonesha namna ushirika unavyoendelea kuwa nguzo muhimu ya maendeleo ya kiuchumi kwa kuwahudumia wakulima na wanaushirika katika nyanja mbalimbali.

Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amepongeza Tume ya Maendeleo ya Ushirika (TCDC), Shirika la Bima la Taifa (NIC) na Shirikisho la Vyama vya Ushirika Tanzania (TFC) kwa kusaini mkataba wa makubaliano ya kiutendaji, akisema hatua hiyo inaonesha dhamira ya dhati ya kumkwamua mkulima kwa kumpatia huduma ya bima ya uhakika itakayomwezesha kutekeleza shughuli zake bila vikwazo.

Naye Mrajis Mkuu wa Vyama vya Ushirika nchini, Benson Ndiege, amesema Kijiji cha Ushirika kimeandaliwa ili kuonesha namna mfumo wa ushirika kupitia vyama vyake unavyoweza kuwahudumia wanaushirika kuanzia uzalishaji, uchakataji na uongezaji thamani wa mazao, pamoja na huduma za kifedha kupitia vyama vya akiba na mikopo na huduma za bima.

Amesema kupitia maonesho hayo, vyama vya ushirika vimepata nafasi ya kuonesha kwa vitendo ubunifu na mchango wake katika kuinua maisha ya wakulima, huku vikionesha huduma na bidhaa mbalimbali zinazotolewa kwa wanachama wake katika mnyororo mzima wa thamani.






Na Mwandishi wetu, Babati

NAIBU Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Regina Ndege ameshiriki kufunga mkutano mkubwa wa Injili mji mdogo wa Gallapo Wilayani Babati Mkoani Manyara, kwa kuwaasa waumini na viongozi wa dini kuombea amani Taifa na kumuombea afya njema Rais Samia Suluhu Hassan ili aweze kuendelea kuingoza vyema Tanzania.

Naibu Waziri Ndege ambaye pia ni Mbunge wa Viti maalum wa Mkoa wa Manyara, ameeleza hayo wakati akifunga mkutano mkubwa wa injili ulioandaliwa na Kanisa la Tanzania Assemblies of God (TAG) Gallapo.

Ameliomba Kanisa kuendelea kuiombea nchi iwe na amani na utulivu pamoja na kumuombea Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt Samia Suluhu Hassan afya njema.

"Ili tuweze kuishi vyema kwa kufanya maendeleo na kuwa na amani kwenye familia na nchi kwa ujumla tunapaswa kuendelea kuomba kwa Mungu atujalie amani na utulivu na pia kumuombea afya njema kiongozi wetu anayeongoza nchi," amesema Naibu Waziri Ndege.

Amewapongeza viongozi wa dini kwa kuendelea kuwa na jukumu la kuiombea nchi na viongozi wake sambamba na kuwaomba waumini kutenda matendo mema ya kumpendeza Mungu.

Mkutano huo umehusisha umoja wa makanisa yote ya Kipentekoste Wilayani Babati na umehitimishwa katika eneo la viwanja vya mpira Gallapo.

Mchungaji wa TAG Gallapo, Steven Konki amemshukuru Naibu Waziri Ndege kwa kutenga muda wake na kuhudhuria kwenye mkutano huo wa Injili.

"Tunakushukuru kwa kuja kwani upendo wako kwetu ni mkubwa na kila wakati umekuwa baraka kwetu, tunaendelea kukuombea afya njema, kuombea amani ya Taifa letu na kumuombea afya njema Rais wetu Dkt Samia ili azidi kutuongoza vyema," amesema Mchungaji Konki.


Mjumbe wa Kamati ya Utekelezaji ya Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT), Mhe. Mariam Abdallah Ibrahim, ameendelea na ziara yake katika Mkoa wa Morogoro, Wilaya ya Mvomero.


Akiwa Wilayani Mvomero, Mhe. Mariam amewashukuru wanachama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) pamoja na wananchi kwa kukiamini chama na kukipa ushindi mkubwa katika Uchaguzi Mkuu.

Katika ziara hiyo, amesisitiza umuhimu wa kuimarisha uhai wa jumuiya kwa kufanya vikao mbalimbali, kuhamasisha ushiriki wa wanawake katika shughuli za chama, pamoja na kuwahimiza wanawake kujitokeza kugombea nafasi mbalimbali za uongozi ndani ya chama.

Aidha, Mhe. Mariam amekagua vikundi vilivyopatiwa mikopo kupitia Halmashauri na kuangalia maendeleo ya miradi yao. Pia amekagua ujenzi wa nyumba ya mtumishi wa UWT na kuchangia kiasi cha Shilingi Milioni Tano (5,000,000) kwa ajili ya kuunga mkono ujenzi huo.

“Tunaendelea kuimarisha jumuiya, kuwawezesha wanawake na kuhakikisha maendeleo yanafika kwa wananchi.”

Mhe. Mariam Abdallah Ibrahim
Mjumbe wa Kamati ya Utekelezaji ya UWT Taifa






 

-ASHIRIKI MAADHIMISHO YA MIAKA 10 YA TARI NA SIKU MAALUM YA USHIRIKA

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi ameitaka Tume ya Maendeleo ya Ushirika kuendelea kufanya usimamizi wa vyama vya ushirika na kutoa miongozo ya kitaalamu kwa vyama vyote nchini.

Makamu wa Rais ametoa wito huo, wakati wa Siku Maalum ya Ushirika katika Maonesho ya Kimataifa ya Nane Nane kwa mwaka 2026, yanayofanyika katika Viwanja vya John Malecela, Nzuguni mkoani Dodoma. 

Amesisitiza Shirika la Ukaguzi na Usimamizi wa Vyama vya Ushirika (COASCO) kuhakikisha linaendelea kufanya ukaguzi wa mara kwa mara kwa vyama vya ushirika kwa lengo la kuhakikisha nidhamu ya matumizi ya fedha, kuzuia ubadhirifu na kuongeza uwazi katika uendeshaji wa vyama hivyo.

 Makamu wa Rais, amesema Ushirika wenye uadilifu ni muhimu sana katika kujenga imani kwa wanachama na kuvutia uwekezaji zaidi. Amesema kuimarika kwa ushirika kunategemea uwajibikaji, uaminifu na uadilifu wa wanachama, viongozi na watendaji wa vyama vya ushirika.

 Makamu wa Rais ametoa wito kwa taasisi za umma na binafsi, wadau wa maendeleo na wadau wote kuipa ushirikiano Tume ya Maendeleo ya Ushirika katika kufanisha utekelezaji wa Kampeni ya "Linda Ushirika, Chagua Uadilifu" iliyozinduliwa hivi karibuni, inayolenga kutokomeza vitendo vya kihalifu ndani ya Ushirika.

Vilevile, Makamu wa Rais ameielekeza Wizara ya Kilimo kupitia Tume ya Maendeleo ya Ushirika kuhakikisha ushirika unaendana na Dira ya 2050 inayoelekeza Vyama vya Ushirika kuwa na mwelekeo wa kibiashara na kuwa kichocheo muhimu cha ujenzi wa uchumi wa viwanda na ukuaji jumuishi wa Taifa. Pia amesisitiza umuhimu wa kutoa elimu na hamasa zaidi kwa wananchi wote ili kujiunga na vyama vya ushirika na kufikia lengo la Mpango wa Maendeleo wa miaka mitano la kufikisha vyama vya ushirika 20,540,850 ifikapo 2030/2031.

Makamu wa Rais amesema katika kukuza sekta ya kilimo na kuongeza mchango wake katika uchumi wa Taifa, Serikali imedhamiria kutoa huduma bora kwa wakulima zikiwemo pembejeo na huduma za ugani kwa wakati. Mathalan, katika kuongeza matumizi ya mbolea nchini, Serikali inaendelea kuimarisha upatikanaji na kuhimiza matumizi ya mbolea kupitia Mpango wa ruzuku ili kuongeza tija na uzalishaji.

Katika hatua nyingine, Makamu wa Rais ameshiriki Maadhimisho ya Miaka 10 ya Taasisi ya Utafiti wa Kilimo (TARI) yaliyofanyika katika Maonesho ya Nane Nane katika Viwanja vya John Malecela mkoani Dodoma.

 Katika maadhimisho hayo, Makamu wa Rais ameipongeza Wizara ya Kilimo, Taasisi ya TARI na wadau wote kwa mchango wao mkubwa katika kipindi cha miaka 10 wa kubuni na kusambaza teknolojia na ubunifu unaoendelea kuleta mageuzi katika sekta ya kilimo na kuboresha Maisha ya wakulima nchini.

Aidha Makamu wa Rais, amewataka watafiti wa Taasisi ya TARI kutafsiri Dira ya Taifa 2050 kuwa matokeo yanayoonekana kupitia tafiti na ubunifu unatoa suluhisho kwa changamoto ya sekta ya kilimo kwa kuongeza tija, ushindani na kuongeza thamani ya mazao. 

Amesema historia inafundisha maendeleo ya ukweli na endelevu yanajengwa kwa kuwekeza katika rasilimali watu kupitia elimu bora, sayansi, teknolojia na ubunifu, hivyo Dira ya Taifa 2050 imeweka utafiti na ubunifu kama sehemu ya nguzo muhimu za kujenga uchumi imara na wenye ushindani.

 Maonesho ya Kimataifa ya Nane Nane kwa mwaka 2026 yanafanyika katika kauli mbiu isemayo “Tambua soko, ongeza tija, kutekeleza Dira 2050”.








NA DENIS MLOWE, IRINGA


MKUU wa Wilaya ya Iringa Benjamin Sitta imezindua rasmi maandalizi ya maadhimisho ya jubilee ya miaka 100 ya Shule ya Sekondari Tosamaganga, huku ikitoa wito kwa wanafunzi wa zamani, wadau wa elimu, taasisi, kampuni na Watanzania wote kushiriki kikamilifu katika kuifanya historia hiyo kuwa ya mafanikio.
Akizungumza na waandishi wa habari wakati wa uzinduzi huo, Mkuu wa Wilaya ya Iringa, Benjamini Sitta, alisema shule hiyo iliyoanzishwa mwaka 1926 imekuwa nguzo muhimu ya elimu bora, maadili na uongozi nchini, hivyo maadhimisho ya miaka 100 yanapaswa kuwa fursa ya kuenzi mchango wake kwa taifa.

Alisema maadhimisho hayo yatafanyika chini ya kauli mbiu isemayo, “Miaka 100 ya Elimu Bora, Maadili, na Uongozi wa Kuigwa,” kauli inayobeba historia ya shule hiyo katika kuzalisha viongozi, wataalamu na wazalendo waliolitumikia taifa kwa uadilifu na weledi.

Sitta alisema ratiba ya maadhimisho imeanza kupangwa ambapo Oktoba 8, 2026 kutafanyika matembezi ya Jubilee Walk pamoja na zoezi la usafi wa mazingira kwa lengo la kuhamasisha afya, uzalendo na utunzaji wa mazingira.

Alisema Oktoba 9 kutafanyika mbio za burudani (Fun Run) zitakazowakutanisha wanafunzi wa zamani wa Tosamaganga, wanafunzi wa sasa, wananchi na wadau mbalimbali, huku kilele cha maadhimisho kikitarajiwa kufanyika Oktoba 10, 2026.

Aliongeza kuwa siku ya kilele itahusisha maonyesho ya historia ya shule, nyaraka na kumbukumbu muhimu, vifaa vya kujifunzia na kufundishia, utoaji wa tuzo za heshima pamoja na shughuli mbalimbali zitakazoonesha urithi mkubwa wa taasisi hiyo.

Alisema maadhimisho hayo hayatakuwa ya kusherehekea historia pekee, bali yataacha alama kupitia utekelezaji wa miradi ya maendeleo ikiwemo kuboresha miundombinu ya shule, ununuzi wa basi la wanafunzi na miradi mingine itakayokubaliwa na wadau.

"Huu ni wakati wa wanafunzi wote wa zamani, marafiki wa Tosamaganga na wadau mbalimbali kushiriki kikamilifu na hata waliopo nje ya nchi tunawakaribisha kuungana nasi kuandika historia nyingine ya shule hii ya kipekee," alisema Sitta.

Aliongeza kuwa Serikali ya Mkoa wa Iringa inaamini maadhimisho hayo yatachochea uchumi wa mkoa kutokana na matarajio ya kupokea maelfu ya wageni watakaotumia huduma za malazi, usafiri, chakula, utalii na biashara nyingine mbalimbali.

Sitta alisema Tosamaganga ni shule ya kihistoria yenye usajili namba moja nchini (S1), jambo linaloifanya kuwa sehemu muhimu ya historia ya elimu Tanzania.

Naye Mwalimu Mkuu wa Shule ya Sekondari Tosamaganga, Laurent Manga, alisema lengo kuu la maadhimisho hayo ni kumshukuru Mungu kwa mafanikio ya shule, kuwakutanisha wanafunzi wa zamani na wadau pamoja na kuhamasisha michango kwa ajili ya kuiboresha taasisi hiyo.

Alisema serikali imekuwa na mchango mkubwa katika maendeleo ya shule hiyo baada ya kutoa zaidi ya shilingi milioni 650 kwa ajili ya ukarabati wa majengo, hatua iliyowezesha wanafunzi kusoma katika mazingira salama na bora zaidi.

Manga alisema kutokana na matokeo mazuri ya kitaaluma, shule hiyo imepewa hadhi ya kuwa shule maalumu (Special School), ambapo sasa inapokea wanafunzi wa kidato cha tano wenye ufaulu wa juu wa alama za pointi 7 hadi 10.

Aidha alisema shule inaendelea kupata huduma muhimu zikiwemo maji, umeme na chakula bila changamoto kubwa, huku akitoa wito kwa wanafunzi wote wa zamani kurejea kushiriki maadhimisho hayo na kuchangia maendeleo ya shule.

"Tunatamani kupata basi la shule ili kuwasaidia wanafunzi katika shughuli mbalimbali za masomo na safari. Hili ni moja ya vipaumbele vyetu katika maadhimisho haya ya miaka 100," alisema Manga.

Kwa upande wake, Mjumbe wa Kamati ya Habari, Hamasa na Matangazo ya maadhimisho hayo, Mwalimu Gayrus Edward Mwakavindi, alisema kamati imeweka lengo la kukusanya shilingi bilioni moja kwa ajili ya kufanikisha maadhimisho pamoja na utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Alisema michango inaweza kutumwa kupitia akaunti ya CRDB yenye jina la Tosa Maganga Jubilee pamoja na njia nyingine za malipo zilizotengwa kwa ajili ya zoezi hilo.

Mwakavindi alisema kamati ya maandalizi imejumuisha walimu waliowahi kufundisha Tosamaganga, wanafunzi wa zamani wa vipindi mbalimbali, viongozi wa serikali, wanasiasa, wanamichezo na wadau wengine wenye mapenzi na shule hiyo.

Aliwahimiza waandishi wa habari kuendelea kutoa ushirikiano katika kuhamasisha wananchi kushiriki maadhimisho hayo ili kuhakikisha historia ya miaka 100 ya Shule ya Sekondari Tosamaganga inaenziwa na kuacha alama kwa vizazi vijavyo.







Top News