📍 Chinangali Park, Dodoma

TAWIRI  imeendelea kutoa elimu  kwa wadau wakiwepo  wananchi ambapo wakulima wamepata elimu ya umuhimu wa wadudu katika  uhifadhi endelevu wa wanyamapori sambamba na mchango wa wadudu katika kilimo ikiwa ni pamoja na uchavushaji.

Vilevile wananchi wamepata uelewa  juu ya juhudi zinazofanywa na TAWIRI chini ya Wizara ya Maliasili na Utalii za kuwahifadhi wanyamapori kwa kutumia taarifa sahihi za kisayansi.

“tunashukuru kwa elimu nzuri, kabla ya elimu hii nilijua wanyamapori wanakaa porini wanajihudumia lakini leo nimepata uelewa  wanyamapori wanatibiwa, wanahesabiwa, wanafuatiliwa mienendo yao kwa kutumia teknolojia” 

amesema  Enderesa Salla miongoni mwa wananchi waliotembelea banda la TAWIRI

TAWIRI tunawakaribisha wananchi na wadau mbalimbali kuja kupata elimu ya sayansi ya wanyamapori  kwa ustawi wa uhifadhi na kukuza Utalii.



Na Said Mwishehe,Michuzi TV


RAIS wa Jamhuri ya Namibia, Dkt. Netumbo Nandi-Ndaitwah amewasili nchini Tanzania kwa ziara ya Kitaifa ya siku tatu kwa mwaliko wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Akiwa nchini Rais Dkt. Nandi-Ndaitwah anatarajiwa kufanya mazungumzo ya uwili na mwenyeji wake, Rais Dkt. Samia kwa lengo la kuimarisha zaidi ushirikiano katika sekta mbalimbali zenye manufaa kwa Wananchi wa Tanzania na Namibia.

Pia Rais Ndaitwah na mwenyeji wake Rais Dk.Samia wanatarajiwa kushuhudia utiaji saini wa hati mbalimbali za makubaliano ya ushirikiano kati ya Nchi hizo mbili.

Aidha pamoja na mambo mengine inaelezwa kwamba ziara hiyo inakwenda kufungua fursa zaidi za kiuchumi kati ya nchi hizo ambazo zimekuwa na urafiki wa kindugu na wa kihistoria kwa muda mrefu.

Akizungumzia ziara hiyo alipokuwa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam wakati wa mapokezi ya Rais Ndaitwah, Balozi wa Tanzania nchini Namibia, Caesar Waitara, amesema ziara hiyo ni ishara ya uhusiano wa muda mrefu na wa kihistoria uliopo kati ya mataifa hayo mawili, huku akisisitiza kuwa ziara hiyo inaleta manufaa makubwa katika utekelezaji wa diplomasia ya uchumi.

Balozi Waitara anasema Rais wa Namibia anaitazama Tanzania kama nyumbani kwake kutokana na historia yake ya kuishi nchini kwa miaka sita alipokuwa mwakilishi wa chama cha SWAPO katika nchi za Afrika Mashariki.

Anabainisha kuwa makao yake yalikuwa katika eneo la Magomeni jijini Dar es Salaam, jambo linaloimarisha zaidi uhusiano wake binafsi na Tanzania.

“Ujio wake unaonyesha jinsi uhusiano kati ya Tanzania na Namibia ulivyo imara na wa muda mrefu. Kila mara anapokuja Tanzania anajisikia kama yuko nyumbani,” anasema Waitara.

Anaeleza kuwa Namibia inaendelea kuthamini mchango wa Tanzania katika harakati za ukombozi wa taifa hilo, hususan kupitia kambi za wapigania uhuru zilizokuwa Kongwa pamoja na msaada wa mafunzo ya kijeshi uliotolewa kwa wapigania uhuru wa Namibia.

Kwa mujibu wa balozi huyo, pamoja na historia ya ukombozi, mataifa hayo sasa yamejikita zaidi katika kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi kupitia biashara, uwekezaji na kubadilishana uzoefu katika sekta mbalimbali za maendeleo.

Waitara anasema Tanzania inaendelea kusukuma mbele ajenda ya diplomasia ya uchumi kupitia balozi zake nje ya nchi kwa lengo la kuvutia uwekezaji na kufungua fursa za biashara.

Anataja uwekezaji wa Watanzania nchini Namibia kuwa ni mfano wa mafanikio ya ushirikiano huo, ambapo baadhi ya Watanzania wameanzisha biashara na taasisi za elimu.

Anabainisha kuwa kuna chuo kikuu nchini Namibia kinachomilikiwa kwa asilimia 100 na Mtanzania, ambacho kinatoa elimu ya shahada, shahada za uzamili na uzamivu, huku kikiwa na zaidi ya wanafunzi 10,000.

Aidha, Watanzania wengine wanaendelea kufanya biashara mbalimbali nchini humo, wakati WanaNamibia wamewekeza Tanzania katika sekta za utalii na mawasiliano.

Katika kuimarisha mahusiano ya kitamaduni, Waitara anasema ubalozi wa Tanzania kwa kushirikiana na Baraza la Kiswahili la Taifa (BAKITA) umeanza kutoa mafunzo ya lugha ya Kiswahili kwa njia ya mtandao nchini Namibia.

Anafafanua wanafunzi 26 walihitimu mafunzo ya awali mwaka jana, huku kundi jipya la wanafunzi 40 likitarajiwa kuanza masomo hivi karibuni.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, akizungumzia ziara ya Rais wa Namibia anasisitiza ni uthibitisho kuwa mahusiano ya kihistoria kati ya mataifa hayo sasa yamepanuka na kuwa ushirikiano mkubwa wa kiuchumi.

Anasema maboresho makubwa yaliyofanyika katika Bandari ya Dar es Salaam yanaifanya Tanzania kuwa lango muhimu la biashara kwa nchi nyingi za ukanda wa Kusini mwa Afrika, jambo linaloweza kuongeza ushirikiano wa kibiashara kati ya Tanzania na Namibia.

Wakati Kamanda wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Jumanne Muliro, anasema mafanikio ya diplomasia ya uchumi hayawezi kupatikana bila kuwepo kwa usalama.

Ananasisitiza kuwa amani na utulivu wa Tanzania ndiyo msingi unaowezesha viongozi wa kimataifa kutembelea nchi na wawekezaji kuendelea kuwekeza.

“Usalama ni mtaji muhimu wa uchumi. Bila usalama hakuna biashara, hakuna uwekezaji wala maendeleo. Ni jukumu la kila mwananchi kuendelea kuilinda amani ya nchi yetu,” anasema Kamanda Muliro.

Ziara ya Rais wa Namibia nchini Tanzania inatarajiwa kuimarisha zaidi ushirikiano wa kihistoria, kiuchumi na kitamaduni kati ya mataifa hayo mawili, huku ikifungua fursa mpya za biashara, uwekezaji na maendeleo kwa wananchi wa pande zote mbili.


Na Chalila Kibuda ,Michuzi TV

SERIKALI imeitaka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kujiandaa mapema kukabiliana na mabadiliko makubwa ya kiuchumi na kiteknolojia yanayotarajiwa katika miaka 30 ijayo, ikieleza kuwa zaidi ya asilimia 70 ya shughuli za kiuchumi zitakuwa zikifanyika kwa njia za kidijitali.

Hayo ameyasema na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Nsubili Joshua, kwa niaba ya Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omary, wakati wa Kongamano la Miaka 30 ya TRA tangu kuanzishwa kwake mwaka 1996, lililoandaliwa na TRA kupitia Chuo cha Kodi.

Joshua alisema mabadiliko ya teknolojia yanayoendelea duniani yanahitaji TRA kuwa mbele ya wakati kwa kuandaa mifumo madhubuti ya usimamizi wa kodi itakayoweza kukusanya mapato kutoka biashara za mtandaoni na huduma zinazovuka mipaka ya nchi.

Alisema pamoja na mafanikio makubwa yaliyopatikana katika kipindi cha miaka 30 ya TRA, bado kuna haja ya kuimarisha mifumo ya kodi ili iendane na kasi ya maendeleo ya uchumi wa kidijitali unaotarajiwa kutawala katika miaka ijayo.

“Katika miaka 30 ijayo zaidi ya asilimia 70 ya shughuli za kiuchumi zitafanyika kwa njia za kidijitali hivyo TRA inapaswa kuwa tayari kuhakikisha mapato ya Serikali yanakusanywa kwa ufanisi bila kuathiri mazingira ya biashara na ubunifu,” amesema Joshua.

Alifafanua kuwa lengo la Serikali si kuzuia maendeleo ya teknolojia, bali kuhakikisha kunakuwa na usawa wa kodi na ulinzi wa mapato ya taifa huku mazingira bora ya uwekezaji na ushindani wa haki yakiendelea kudumishwa.

Aidha, aliitaka TRA kuongeza uwekezaji katika matumizi ya akili mnemba (AI), uchambuzi wa takwimu na mifumo ya ufuatiliaji wa miamala kwa wakati halisi ili kubaini mianya ya ukwepaji kodi na kuimarisha uwazi katika ukusanyaji wa mapato.

Joshua alisema matumizi ya teknolojia hizo yatasaidia kugundua udanganyifu mapema, kupunguza mawasiliano yasiyo ya lazima kati ya walipakodi na maafisa wa kodi pamoja na kuongeza ufanisi wa utoaji huduma.

Pia aliitaka TRA kuendelea kubuni mifumo rahisi ya usajili, ukadiriaji na ulipaji kodi kwa sekta isiyo rasmi ikiwemo wafanyabiashara wadogo na wakulima, ili kupanua wigo wa walipakodi na kuongeza mapato ya ndani.

Alisema mafanikio ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 yatategemea kwa kiasi kikubwa uwezo wa nchi kukusanya mapato ya ndani na kuyasimamia kwa ufanisi, jambo linaloifanya TRA kuwa na jukumu muhimu katika safari ya maendeleo ya taifa.

Joshua alisisitiza kuwa ushirikiano kati ya TRA, wafanyabiashara, watafiti na wadau wengine wa kodi ni muhimu katika kujenga mfumo wa kodi unaoendana na mahitaji ya uchumi wa kisasa na kuhakikisha Tanzania inanufaika kikamilifu na mapinduzi ya teknolojia yanayoendelea duniani.
Kamishina Mkuu wa TRA CPA Yusuph Mwenda akitoa maelezo kuhusiana tangu kuanzishwa mamlaka ya Mapato katika kongamano la miaka 30 tangu Kuanzishwa lililofanyika Ukumbi wa Serena ,jijini Dar es Salaam.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha Nsubili Jushua akizungumza kwa niaba ya Waziri wa Fedha Balozi Khamis Mussa Omary wakati akizindua Kongamano la Miaka 30 ya Mamlaka ya Mapato (TRA) lililofanyika Ukumbi wa Serena Jijini Dar es Salaam.

Mkuu wa Chuo cha Kodi Profesa Isaya Jairo akizungumza kuhusiana na kuratibu Kongamano hilo kwa lengo kukutanisha wadau kujadiliana miaka 30 ijayo juu utendaji wa TRA.jijini Dar es Salaam.



Picha za pamoja za Makundi katika kongamano la TRA


- Mikopo ya mifugo NMB yavuka Sh180 bilioni.

Ubena Zomozi; Benki ya NMB imetoa zaidi ya Sh180 bilioni kufadhili wafugaji na biashara katika mnyororo wa thamani wa mifugo, ikiwemo unenepeshaji, uzalishaji wa malisho, ununuzi wa mbegu bora na ujenzi wa miundombinu ya kisasa.

Afisa Mkuu wa Wateja Binafsi na Biashara wa NMB, Filbert Mponzi, alisema hayo katika ufunguzi wa Tri-Nations Livestock Expo 2026 uliofanywa na Waziri Mkuu, Dk. Mwigulu Nchemba, katika viwanja vya Mbogo Ranches, Ubena Zomozi, Chalinze. NMB ni mdhamini mkuu kwa mwaka wa nne mfululizo.

Mponzi alisema mikopo hiyo inatolewa kwa riba nafuu ya asilimia tisa, huku mkakati wa NMB wa agribusiness na agri-wholesale ukilenga kufadhili wafugaji, wazalishaji wa malisho, wanunuzi, wasindikaji na biashara kubwa katika sekta hiyo.

Dk. Nchemba aliwataka wafugaji kutumia elimu na teknolojia inayopatikana katika maonesho hayo kukabiliana na uhaba wa malisho na kuongeza tija.

NMB imesema itaendelea kutoa elimu ya fedha, ushauri wa biashara, mikopo na bima kupitia matawi 248, mawakala zaidi ya 75,000 na huduma za kidijitali ili kusogeza huduma karibu zaidi na wafugaji nchini.

Waziri Mkuu, Dk. Mwigulu Nchemba, akisikiliza maelezo kutoka kwa Afisa Mkuu wa Wateja Binafsi na Biashara wa NMB, Filbert Mponzi, kuhusu mikopo, elimu ya fedha na huduma za kibenki kwa wafugaji alipotembelea banda la NMB katika Tri-Nations Livestock Expo 2026, Mbogo Ranches, Ubena Zomozi wilayani Chalinze, mkoani Pwani. 







 


Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) imeungana na Taasisi mbalimbali za umma kushiriki katika Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayofanyika katika viwanja vya Chinangali Park, jijini Dodoma kuanzia, Juni 16, 2026.

Katika maonesho hayo, TCAA inatoa elimu kwa wananchi kuhusu majukumu yake ya msingi, yakiwemo udhibiti wa shughuli zote za usafiri wa anga nchini. Hii inajumuisha pia usimamizi wa matumizi ya droni, ambalo ni eneo linalokua kwa kasi na kuhitaji ufuatiliaji wa karibu siyo tu kwa ajili ya usalama wa anga, bali pia kulinda faragha ya watu na kuepusha matumizi ya vifaa hivyo katika maeneo yasiyoruhusiwa kisheria, kama vile maeneo ya kijeshi, taasisi za serikali, na miundombinu nyeti.

Huduma nyingine zinazotolewa na TCAA ni pamoja na utoaji wa huduma za uongozaji ndege kwa ajili ya kuhakikisha usalama wa safari za anga ndani ya eneo la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Aidha, Mamlaka hiyo inatumia fursa hiyo kuwahamasisha vijana na wadau wa sekta ya usafiri wa anga kuchangamkia fursa za mafunzo zinazotolewa na Chuo cha Usafiri wa Anga Tanzania (CATC), kinachomilikiwa na TCAA. Mafunzo hayo yanalenga kuongeza idadi ya wataalamu wa ndani katika sekta muhimu ya usafiri wa anga.

Maadhimisho ya mwaka huu yanaongozwa na kaulimbiu: “Kuchochea uwajibikaji Jumuishi kwa Huduma Endelevu” ikisisitiza umuhimu wa matumizi ya teknolojia katika kuboresha huduma kwa wananchi na kuimarisha uwajibikaji katika utumishi wa umma.

Wiki ya Utumishi wa Umma huadhimishwa kila mwaka ili kutambua mchango wa watumishi wa umma katika maendeleo ya taifa. Maadhimisho ya mwaka huu yanatarajiwa kufikia kilele chake tarehe 23 Juni 2026.
Meneja wa TCAA Kituo cha Dodoma Aswile Kamendu (katikati) akitoa maelezo kwa Mkurugenzi wa Ufuatiliaji na Tathmini kutoka Wizara ya Uchukuzi Devota  Gabriel aliyefika katika banda la Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) kwenye maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayofanyika katika viwanja vya Chinangali Park, jijini Dodoma. 
Mkurugenzi wa Huduma za Usafiri kutoka Wizara ya Uchukuzi Biseko Chiganga  akisaini kitabu katika banda la Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) kwenye maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayofanyika katika viwanja vya Chinangali Park, jijini Dodoma. 
Afisa Rasilimali Watu TCAA Lucy Ngowo (wa pili kulia) akikabidhi zawadi kwa Mkurugenzi wa Huduma za Usafiri Wizara ya Uchukuzi ambaye pia ni Mjumbe wa Bodi Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) Biseko Chiganga
Mkurugenzi wa Huduma za Usafiri kutoka Wizara ya Uchukuzi Biseko Chiganga akiwa kwenye picha pamoja na watumishi wa  Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) alipotembelea banda la Mamlaka hiyo kwenye maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayofanyika katika viwanja vya Chinangali Park, jijini Dodoma. 

Baadhi ya wafanyakazi wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) wakiendelea kutoa elimu katika Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yaliyofanyika kwenye Viwanja vya Chinangali jijini Dodoma.

Ofisi ya Waziri Mkuu pamoja na wadau wa maafa nchini katika Kikao cha Jukwaa la Taifa la Wadau wa Usimamizi wa Maafa kilicholenga kupitia na kuthibitisha Mwongozo wa Urejeshaji Hali Baada ya Maafa, Mwongozo wa Uendeshaji na Uratibu wa Uhawilishaji Fedha kwa Walioathirika wa Maafa, pamoja na Mfumo wa Usimamizi wa Taarifa za Maafa (DMIS) tarehe 19 Juni, 2026 Jijini Dodoma.


DAR ES SALAAM, Juni 18, 2026 – Katibu Msaidizi wa Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Kanda Maalum, Bi. Elizabeth Komba, amewataka viongozi nchini kuwa mfano wa maadili mema kwa maneno, matendo na mwenendo wao wa kila siku ili kuimarisha utawala bora na kujenga imani ya wananchi kwa taasisi za umma.
Bi. Komba alitoa kauli hiyo wakati akifungua mafunzo ya maadili kwa viongozi yaliyofanyika katika Ukumbi wa Tume ya Ushindani jijini Dar es Salaam tarehe 18 Juni 2026.

Alisema Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma, inaendelea kuhamasisha ushiriki wa wananchi na viongozi katika kusimamia na kukuza maadili ili kuimarisha uwajibikaji na utoaji bora wa huduma katika sekta ya umma.

“Viongozi wanapaswa kuwa kioo cha jamii kwa kuzingatia maadili katika maneno na matendo yao. Kwa kufanya hivyo, wataweza kusimamia maadili katika taasisi wanazoziongoza na kuhamasisha watumishi wengine kufuata misingi hiyo,” alisema Bi. Komba.

Aidha, alibainisha kuwa maadili na uadilifu ni nguzo muhimu katika maendeleo ya taifa lolote duniani, kwani humjengea kiongozi heshima, uaminifu na kuthaminiwa na wananchi anaowahudumia.

Alisisitiza kuwa viongozi wanapaswa kutenda haki kwa wote bila ubaguzi, upendeleo au misingi yoyote inayoweza kuathiri utoaji wa huduma kwa wananchi.

Bi. Komba alisema mafunzo hayo yanalenga kuwajengea viongozi uwezo wa kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa, hatua itakayosaidia kuimarisha utoaji wa huduma za umma na kuongeza imani ya wananchi kwa taasisi za Serikali.

Aliongeza kuwa viongozi wenye maadili na uadilifu ni msingi wa maendeleo endelevu, huku akiwataka washiriki wa mafunzo hayo kuyatumia maarifa waliyopata kuboresha utendaji kazi katika maeneo yao ya kazi.

Mafunzo hayo ni sehemu ya jitihada za Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma za kuendelea kuimarisha misingi ya maadili, uwajibikaji na uadilifu miongoni mwa viongozi wa umma nchini.









Rais wa Jamhuri ya Namibia, Mhe. Dkt. Netumbo Nandi-Ndaitwah, amewasili nchini kwa Ziara ya Kitaifa ya siku tatu kuanzia tarehe 19 hadi 21 Juni 2026, kwa mwaliko wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), jijini Dar es Salaam, Mhe. Dkt. Nandi-Ndaitwah alipokelewa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo, pamoja na viongozi wengine waandamizi wa Serikali. Katika mapokezi hayo pia alikuwepo Balozi wa Jamhuri ya Namibia nchini Tanzania, Mhe. Gabriel Sinimbo.

Ziara hiyo inafanyika katika kipindi ambacho Tanzania na Namibia zinaendelea kuimarisha uhusiano wao wa kihistoria uliojengwa katika misingi ya mshikamano wa harakati za ukombozi wa Afrika, urafiki wa muda mrefu na ushirikiano wa karibu katika nyanja mbalimbali za maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Akiwa nchini, Mhe. Rais Nandi-Ndaitwah anatarajiwa kufanya mazungumzo ya uwili na mwenyeji wake, Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa lengo la kuimarisha zaidi ushirikiano katika sekta mbalimbali zenye manufaa kwa wananchi wa Tanzania na Namibia. Viongozi hao pia wanatarajiwa kushuhudia utiaji saini wa hati mbalimbali za makubaliano ya ushirikiano kati ya nchi hizo mbili.

Ziara hii ya kwanza ya Kitaifa ya Rais Nandi-Ndaitwah nchini Tanzania tangu alipoingia madarakani inaashiria dhamira ya pamoja ya Tanzania na Namibia ya kuendeleza ushirikiano wa kimkakati, kuimarisha diplomasia ya uchumi, pamoja na kukuza biashara na uwekezaji kwa manufaa ya pande zote mbili.

Ziara hii pia inatarajiwa kutoa fursa ya kuenzi historia ya ushirikiano wa ukombozi kati ya Tanzania na Namibia, huku ikifungua ukurasa mpya wa ushirikiano katika nyanja mbalimbali za maendeleo kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho cha wananchi wa mataifa hayo mawili.



Na Karama Kenyunko, Michuzi TV

Mkurugenzi wa Uendeshaji wa MSI Tanzania, Dkt. Stephen Mutegeki, amesema utekelezaji wa Programu ya Scaling Up Family Planning (SuFP) umeonyesha kuwa maendeleo makubwa yanawezekana pale wadau mbalimbali wanaposhirikiana katika kufikia malengo ya pamoja.

Akizungumza katika kongamano la kujifunza na kutathmini mafanikio ya programu hiyo lililofanyika jijini Dodoma, Dkt. Mutegeki alisema MSI Tanzania itaendelea kushirikiana na serikali na wadau wengine kuhakikisha mafanikio yaliyopatikana yanaendelezwa na kwamba huduma bora na zenye usawa za afya ya uzazi zinaendelea kuwafikia wananchi wote.

Kwa upande wake, Naibu Mkurugenzi wa Maendeleo wa Ubalozi wa Uingereza nchini Tanzania, Will Guest, alisema Serikali ya Uingereza itaendelea kuunga mkono juhudi za kuboresha afya ya uzazi na haki za wanawake na wasichana.

Alisema kupitia SuFP, zaidi ya wanawake na wasichana milioni 5.2 walifikia huduma za uzazi wa mpango, hatua iliyosaidia kuzuia zaidi ya vifo vya wajawazito 6,500 na mimba zisizotarajiwa milioni 8.3.

Akizungumza kwa niaba ya washirika wa utekelezaji, Mwakilishi Mkazi wa UNFPA nchini, Mark Bryan Schreiner, alisema mafanikio ya programu hiyo yamethibitisha kuwa maendeleo makubwa yanawezekana pale serikali, watoa huduma, washirika wa maendeleo na jamii wanaposhirikiana.

Kwa mujibu wa washirika hao, mafanikio yaliyopatikana kupitia SuFP yametokana na ushirikiano wa karibu kati ya Serikali na wadau mbalimbali, wakiwemo MSI Tanzania, UNFPA, Serikali ya Uingereza kupitia FCDO, EngenderHealth na Pathfinder International.

Programu ya SuFP iliyotekelezwa kuanzia mwaka 2017 hadi 2026 kwa ufadhili wa Serikali ya Uingereza kupitia FCDO, ilitekelezwa kwa ushirikiano wa Serikali ya Tanzania na taasisi za EngenderHealth, UNFPA, MSI Tanzania na Pathfinder International.

Mkurugenzi uendeshaji wa MSI Dkt. Stephen Mutegeki






Top News