Na Mwandishi wetu, Simanjiro


WAKUU wa shule za sekondari na msingi wilayani Simanjiro mkoani Manyara, wamejengewa uwezo wa kuandaa taarifa za shule kutokana na kasi ya ukuaji na kuongezeka kwa matumizi ya sayansi na teknolojia ulimwenguni.

Wakuu wa shule 23 za sekondari, 110 wa msingi wa shule za serikali na binafsi wamejengewa uwezo wa kuandaa taarifa za shule ili kurahisisha utoaji na upatikanaji wa wake kupitia serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan kupitia Wizara ya Elimu.

Afisa elimu ya awali na msingi wa Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro, Darius Daudi Limandola amesema walimu hao wamepata mafunzo hayo ya uandaaji wa taarifa za shule kwenye vituo vitatu vya Orkesumet, Terrat na Mirerani.

Limandola ameeleza kwamba mafunzo hayo ya mfumo wa utoaji wa taarifa za kielimu kupitia mfumo wa kidigitali (School Information System) una lengo la kurahisisha utoaji na upatikanaji wa taarifa za shule husika kwa wakati.

Ameeleza kwamba mfumo huo unafanyakazi katika kutoa taarifa za kielimu za shule husika kila siku ikiwemo hali ya miundombinu ya shule, utekelezaji wa lishe kwa wanafunzi, hali ya watumishi na upatikaji wa huduma nyingine za kijamii hususani maji na umeme.

Amesema wanufaika wa mafunzo hayo ni wakuu 23 wa shule za sekondari, walimu wakuu 110 wa shule za msingi, maafisa elimu kata, walimu wa taaluma na takwimu na maafisa elimu ngazi ya wilaya.

Amewataka walimu wakuu na wakuu wa shule kusimamia utekelezaji wa mfumo huo mara moja baada ya shule kufunguliwa Januari 13, 2026 ambapo utairahisishia serikali kufanya maboresho na maamuzi sahihi katika shule husika kwa wakati.

Mmoja wa wawezeshaji wa mafunzo hayo, afisa elimu vifaa na takwimu wa halmashauri ya wilaya hiyo, Abdalah Hamis amesema walimu hao wamejengewa uwezo kwa muda wa siku mbili na kisha watakwenda kuwaelekeza walimu waliobaki katika shule zao.

"Mafunzo yamefanyika katika vituo vitatu vya Orkesumet shule ya sekondari Simanjiro, shule ya sekondari Terrat na shule ya awali na msingi Glisten Mirerani, ambayo yameanza juu kwa wachache watakaokwenda kuwafundisha wengi," amesema Hamis.

Mmoja wa washiriki wa mafunzo hayo, mkuu wa shule ya sekondari Tanzanite, Jude Samwel Mziray amesema mfumo huo ni mzuri kwani wanaaachana na mtindo wa kuingiza taarifa kwenye makaratasi na kuweka katika mfumo wa kiteknolojia.

"Mfumo huo unarahisisha kwani unatoa taarifa ya shule hadi ngazi ya kata, kisha wilaya hadi ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) tofauti na tulivyozoea mwanzo kujaza katika makaratasi," amesema Mziray.

Mwalimu mkuu wa shule ya msingi Naepo, kata ya Naisinyai, Simon Isack Magembe amesema mafunzo hayo yanawajengea uwezo zaidi wa kuboresha taarifa kwa matumizi sahihi.

Mwalimu Magembe amesema ujuzi walioupata wa kuandaa taarifa za mfumo huo umewarahisishia utendaji kazi wao tofauti na awali.



 Yas imeendelea na dhamira yake ya kuwekeza kwenye sekta ya elimu na kukuza vipaji vya vijana wa Kitanzania kupitia udhamini wa wanafunzi kumi mahiri waliochaguliwa kushiriki Kambi Maalum ya Mafunzo ya Hisabati Kigali, Rwanda kuanzia Januari 6 hadi 22, 2026.

Kambi hiyo ya kitaaluma, inayoandaliwa na African Olympiad Academy (AOA) kwa ushirikiano na MIT–Africa, inalenga kuwaandaa wanafunzi wenye vipaji kutoka mataifa mbalimbali ya Afrika kwa ajili ya Mashindano ya Pan-African Mathematics Olympiad (PAMO) yanayotarajiwa kufanyika Juni mwaka huu.

Kupitia taarifa iliyotumwa kwenye vyombo vya habari, Afisa Mkuu wa Udhibiti Yas, Bi. Sylvia Balwire, alisema udhamini huo ni sehemu ya mkakati mpana wa kampuni katika kuendeleza elimu, ubunifu na teknolojia nchini.

“Kupitia udhamini huu, tunaonyesha msimamo wetu wa muda mrefu wa kukuza elimu na kutengeneza kizazi kijacho cha watafiti, wavumbuzi na viongozi wa teknolojia. Somo la Hisabati ndiyo injini ya uchumi wa kidijitali, ubunifu na utatuzi wa changamoto za kisasa. Kwa kuwaunga mkono wanafunzi hawa, tunawekeza moja kwa moja kwenye mustakabali wa taifa letu,” alisema Bi. Balwire.

Aliwapongeza wanafunzi wote waliochaguliwa, akibainisha kuwa uteuzi wao unaakisi uwezo, nidhamu na kujituma kwa kiwango cha juu katika somo la hisabati.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa AOA, Arun Shanmuganathan, alieleza kufurahishwa kwake na ushiriki wa wanafunzi kutoka Tanzania ambao wamepata nafasi ya kuungana na wenzao mahiri kutoka Rwanda, Uganda, Kenya, Botswana, Namibia, Afrika Kusini na Nigeria ambao tayari wanasoma katika taasisi hiyo.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa MIT–Africa, Ari Jacobovits, alisema uwezo mkubwa ulioonekana kwa wanafunzi hao ndio sababu ya MIT kuwekeza kwa kina katika maendeleo yao, popote pale safari yao ya baadaye itakapowapeleka.

Wakati huohuo, Mwenyekiti wa Chama cha Hisabati Tanzania (CHAHITA), Dkt. Said Sima, alitoa shukrani kwa Yas kwa mchango wake endelevu katika kukuza vipaji vya vijana na kuinua taaluma ya hisabati nchini.

Wanafunzi hao 10, ambao tayari wamesafiri kuelekea Rwanda kwa maandalizi haya muhimu ya kitaaluma na kimashindano, wanatoka maeneo mbalimbali ya Tanzania na wanawakilisha shule tofauti ikiwemo Ilboru Arusha, St. Francis Mbeya, Feza, Marian, Mahina, St. Monica Arusha na Mbeya Secondary.






Na Said Mwishehe,Michuzi TV

KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi( CCM) Dk.Asha-Rose Migiro ametoa mwito kwa viongozi wa ngazi mbalimbali wakiwemo Wabunge na Mawaziri kushiriki katika vikao vya mashina na matawi vinavyoitishwa katika maeneo yao.

Akizungumza leo Januari 13 wakati akihitimisha ziara yake ya mkoa wa Dar es Salaam kwa kufanya kikao kazi na viongozi wa CCM katika ngazi ya mashina pamoja na mabalozi Wilaya ya Ilala ameendelea kusisitiza umuhimu wa viongozi wa kitaifa wa Chama hicho kushiriki mikutano ya ngazi ya mashina na matawi.


 “Tumesema  mabalozi wetu mnafanya kazi nzuri  kwani mnaitisha mikutano katika mashina yenu ,hivyo tunapenda kutoa mwito mikutano hii isiwe kwa watu ambao wako katika ngazi ya mashina peke yake au ngazi ya tawi peke.


 “Viongozi wa kitaifa tunao wabunge katika mashina yetu , tunao mawaziri katika mashina yetu yetu.Nitoe mwito kwamba wawe sehemu ya mikutano  hii kwasababu kwa hakika hakuna anayeanzia juu wote tunaanzia kwenye mashina yetu.

“Kwahiyo iwe ni mfano kwa viongozi wetu kuwa sehemu mikutano ile ambayo inaitishwa na mabalozi wetu kwa maana hiyo tutakwenda kadri tunavyoendelea baada ya kupata taarifa ,kupata muhatasari wa yale yanayoendelea tupate kujua ni namna gani tujiimarishe zaidi.

Amesisitiza viongozi wanaposhiriki kwenye vikao ndipo wanapata nafasi ya kutazama changamoto zinazowakabili kama chama lakini na changamoto zinazoikabili jamii yetu na Chama Cha Mapinduzi kina wajibu wa kuzichukua changamoto hizo na kuzifikisha kwenye ngazi za juu.

“Ili  kwa pamoja na kwa kushirikiana nanyi mabalozi kwa kupata ushauri wenu kwa kupata nasaha zenu tuweze kuwapatia wananchi majibu ya changamoto zinazowakabili kwani wametupa dhamana ya uongozi

Kwa upande mwingine Dk.Migiro amezungumzia muelekeo wa Chama Cha Mapinduzi kimkakati katika kuendelea kuimarisha uhai wa chama hicho ambapo amefafanua mabalozi pamoja na kufanya kikao pia waendelee kuweka kumbukumbu za wanachama wao.

“Tumeambiwa hapa mashina ni sehemu muhimu sana ya usalama wa jamii yetu na usalama wa Taifa letu hivyo tutakuwa na wajibu wa kuhakikisha watu ambao tunaishi nao tunajua wanafanya nini na tunajua yale wanayoyafanya yanakuwa salama kwa Taifa letu 

“Tunajua pia hivi sasa balozi wa shina anaweza kuwa na nyumba nyingi sana hivyo kupitia vikao vyetu tutaangalia ni namna gani balozi wa shina apate mzigo ambao anaweza kuubeba ili twende kwa pamoja kuhakikisha chama chetu kinaendelea kuwa chama kiongozi na kinaendelea kushika dola kwa manufaa ya taifa letu.”























-Asisitiza mabalozi kupandisha bendera za chama kwenye maeneo yao.

-Asema chama kinawajali na kuwathamini mabalozi.

Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dkt. Asha-Rose Migiro, amesema maendeleo ya kweli kwa wananchi huanzia katika mashina ya Chama hicho, akisisitiza kuwa jitihada zote za maendeleo ya kijamii na kiuchumi hupata nguvu kupitia uongozi wa ngazi za chini.

Dkt. Migiro ambaye ni Katibu Mkuu wa kwanza mwanamke tangu chama hicho kianzishwe, amesema hayo katika mkutano wake na Mabalozi wa Mashina wa CCM katika Wilaya ya Ilala, ikiwa ni hitimisho la ziara yake katika Mkoa wa Dar es Salaam yenye lengo la kuimarisha uhai wa CCM kuanzia kwenye mashina Kwa kauli mbiu ya "Shina lako linakuita".

Akizungumza na Mabalozi hao amesema mashina ndiyo sehemu ya kwanza ya wananchi kushiriki kikamilifu katika mchakato wa maendeleo, kwa kuwa ndiko wanakotoka wananchi wenyewe na ndiko changamoto zao halisi zinapojadiliwa.

Ameeleza kuwa mahusiano kati ya maendeleo ya jamii na maendeleo ya kisiasa hayawezi kutenganishwa, kwa kuwa mashina imara huwezesha utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwa uwazi, ushirikishwaji na uwajibikaji, jambo linaloongeza imani ya wananchi kwa Chama.

Ameongeza kuwa viongozi wa mashina wana wajibu mkubwa wa kusimamia utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika maeneo yao, akisema uangalizi wa karibu wa miradi hiyo ndio msingi wa maendeleo yenye tija kwa wananchi.

Aidha, Mwanadiplomasia huyo, amesema Mwenyekiti wa CCM, Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amepongeza kazi kubwa inayofanywa na mabalozi hao wa mashina na kwamba chama kitaendelea kuthamini mchango wao mkubwa kwenye mashina.























Wadau mbalimbali wakipata Elimu katika banda la Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) wakati wa maonesho kwenye siku maalum ya Wataalamu wa Uhasibu (NBAA Career Day)

*****************

Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) leo imeshiriki katika maonyesho maalum yaliyoandaliwa na Bodi ya Taifa ya Uhasibu na Ukaguzi (NBAA) kwa ajili ya kuadhimisha Siku ya Wataalamu wa Uhasibu. Maonyesho hayo yamefanyika katika viwanja vya jengo la Mhasibu Posta, jijini Dar es Salaam.

Ushiriki wa TEA katika maonyesho hayo ni sehemu ya jitihada za Mamlaka katika kutangaza shughuli zake pamoja na kuimarisha uhusiano na wadau mbalimbali wa sekta ya elimu kutoka taasisi tofauti.

Kupitia maonyesho hayo, TEA ilitumia fursa hiyo kutoa elimu kwa umma kuhusu majukumu ya Mfuko wa Elimu wa Taifa unaosimamiwa na Mamlaka hiyo pamoja na mchango wa mfuko huo katika kusaidia jitihada za Serikali za kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia nchini.

Akizungumza wakati wa maonyesho hayo Afisa Mawasiliano wa TEA Bi. Eliafile Solla, aliwahimiza wadau wa elimu kushirikiana na Mfuko wa Elimu wa Taifa kwa kutoa michango mbalimbali itakayoongeza uwezo wa mfuko huo kufadhili miradi ya elimu katika maeneo mbalimbali nchini.

Bi. Solla alisema kuwa, lengo kuu la Mfuko wa Elimu wa Taifa unaosimamiwa na TEA ni kuhakikisha kila mtoto wa Kitanzania anapata elimu bora na kwa usawa bila kujali mazingira au hali ya kiuchumi anayotoka.

Kutokana na ushiriki wake mahususi na mchango wake katika maonyesho hayo, Bodi ya Taifa ya Uhasibu na Ukaguzi (NBAA) imeitunuku Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) cheti maalum cha shukrani na utambuzi.

Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) ni taasisi ya umma iliyo chini ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia inayosimamia Mfuko wa Elimu wa Taifa wenye lengo la kukusanya rasilimali fedha na vifaa kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya elimu, ikiwemo ujenzi wa madarasa, mabweni, maabara za Sayansi na nyumba za walimu, ili kuongeza upatikanaji wa elimu bora kwa usawa nchini.
Mdau akipatiwa elimu katika banda la Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) na Bi. Eliafile Solla wakati wa maonesho na kongamano maalum la Siku ya Wataalamu wa Uhasibu Jijini Dar es Salaam
Mdau wa sekta ya Elimu CPA Victorius Kamuntu akiongea na maafisa wa Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) alipotembelea banda la Mamlaka hiyo wakati wa maonesho na kongamano maalum la Siku ya Wataalamu wa Uhasibu Jijini Dar es Salaam.
Wadau na walaalamu wa Uhasibu wakifurahia picha ya pamoja na maafisa wa TEA walipotembelea banda la Mamlaka hiyo wakati wa maonesho na kongamano la Siku ya wataalamu wa Uhasibu Jijini Dar es Salaam

Afisa Uhusiano na Mawasiliano kutoka TEA Bi. Eliafile Solla akipokea cheti cha shukrani na Utambuzi katika maonesho na kongamano la Siku Maalum ya Wataalamu wa Uhasibu Jijini Dar es Salaam
Bi. Eliafile Solla, Afisa Uhusiano kutoka TEA akitoa Elimu kwa mdau aliyetembelea banda la Mamlaka hiyo wakati wa maonesho na maadhimisho ya Siku ya Wataalamu wa Uhasibu Jijini Dar es Salaam


Bi. Bestina Magutu, Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano kwa Umma kutoka Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) akitoa elimu kwa mdau aliyetembelea banda la TEA kwenye maonesho yaliyoandaliwa na Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi
Mdau akisaini kitabu cha wageni katika banda la Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA), wakati wa maonesho na kongamano maalum la Siku ya Wahasibu Jijini Dar es Salaam

Top News