MWENYEKITI wa Bodi ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), Jaji Mshibe Ali Bakari, amezitaka sekta zote nchini kutumia ipasavyo taarifa za hali ya hewa katika kufanya maandalizi ya kisekta ya kukabiliana na athari zinazoweza kusababishwa na uwepo wa El Niño.

Jaji Mshibe aliyasema hayo wakati akifungua Mkutano wa 25 wa kujadili Utabiri wa Msimu wa Mvua za Vuli, Oktoba hadi Disemba 2026, uliofanyika jijini Dodoma hivi karibuni.

“Tunapojiandaa kupokea taarifa ya utabiri wa mvua za Vuli, Oktoba hadi Disemba 2026, ni muhimu kila mmoja wetu kuwa na jukumu la kufuatilia kwa karibu na kuelewa taarifa hizo ili kuanza maandalizi ya hatua za kuchukua katika kukabiliana na athari za hali ya hewa zinazotarajiwa kujitokeza katika sekta yake, kwa kutambua kuwa upo uwezekano mkubwa kwa El Niño kuendelea kuimarika kuelekea mwishoni mwa mwaka 2026,” alisisitiza Jaji Mshibe.

Jaji Mshibe aliongeza kuwa Tanzania, kama ilivyo kwa nchi nyingine duniani, inaendelea kukabiliana na athari za mabadiliko ya hali ya hewa yanayodhihirishwa kupitia ongezeko la joto, ukame, upepo mkali, vimbunga na vipindi vya mvua kubwa vinavyoweza kusababisha mafuriko, hivyo amewataka wadau wasiishie katika kupokea taarifa za utabiri wa hali ya hewa, bali wazitumie katika kufanya maamuzi yanayozingatia mazingira ya sekta na maeneo yao.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi, Dkt. Ladislaus Chang’a, alisema TMA imeendelea kuboresha utoaji wa taarifa za hali ya hewa, ikiwemo kuandaa utabiri mahususi kwa maeneo madogo kwa wilaya 86 zilizopo katika mikoa inayopata mvua za Vuli, hatua inayolenga kuhakikisha kila wilaya na sekta husika zinaweza kutumia taarifa za hali ya hewa katika kufanya maamuzi na kupanga shughuli zao.

Aidha, Dkt. Chang’a alimalizia kwa kusisitiza kuwa taarifa za utabiri na tahadhari zinapaswa kuzingatiwa katika sekta zote za kiuchumi na kijamii, kwa lengo la kuongeza tija na kupunguza madhara yanayoweza kusababishwa na hali mbaya ya hewa itakayotokana na uwepo wa El nino nchini.

“Nitumie fursa hii kuwajulisha kuwa mwaka huu 2026 tunakabiliwa na changamoto ya El Nino ambayo inatarajiwa kuendelea kuimarika kuelekea mwishoni mwa mwaka na hivyo kuchagiza mvua za VULI, hivyo basi matumizi sahihi na kwa wakati ya taarifa za hali ya hewa ni muhimu kwa Kila sekta katika kukabiliana na changamoto hii”. Alisema Dkt.Chang’a.

Naye, mwakilishi wa wadau mbalimbali kutoka Zanzibar, Makame Makame, Mkurugenzi wa kamisheni ya kukabiliana na maafa Zanzibar, Alisema "Utabiri wa hali ya hewa ni jambo moja muhimu mno hasa katika kipindi cha El -Nino ambapo jamii na sekta zote muhimu zinahitaji kujikinga, kujiandaa, kukabiliana na majanga au maafa yanayoweza kutokea sambamba na kurejesha hali baada ya maafa".

Mkutano huo uliobeba kaulimbiu: “Kupunguza Pengo la Uelewa wa Tahadhari za Hali ya Hewa kwa Pamoja.” ulihusisha pia utoaji wa mrejesho kutoka kwa wadau kuhusu utabiri wa msimu wa mvua za Masika uliokuwa na usahihi wa asilimia 94.1.

TMA inatarajia kutoa rasmi utabiri wa msimu wa mvua za Vuli 2026 tarehe 18 Agosti 2026.









Na Mwandishi Wetu.
GEITA Gold Mining Limited (GGML) imetenga takribani Sh bilioni 1.2 kwa kipindi cha miaka mitatu kusaidia matibabu ya watoto 300 wenye magonjwa ya moyo nchini, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuongeza upatikanaji wa huduma za kibingwa kwa watoto ambao familia zao zinaweza kushindwa kumudu gharama za matibabu.

Kupitia makubaliano yaliyosainiwa leo katika ofisi za makao makuu ya GGML mkoani Geita, kati ya kampuni hiyo na Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI), GGML itatoa takribani Sh milioni 400 kila mwaka kusaidia matibabu ya watoto 100 wenye matatizo ya moyo, hivyo kufikisha jumla ya watoto 300 ndani ya miaka mitatu. Ushirikiano huo umefikiwa kwa uratibu wa Global Medicare ya jijini Dar es Salaam.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa GGML, Ashraf Suryaningrat, amesema uamuzi wa kampuni kuunga mkono mpango huo ulifikiwa baada ya kupitia mchakato wa kina wa tathmini unaotumika katika miradi yote ambayo kampuni inaombwa kuisaidia.

“Tunatazamia ushirikiano wa miaka mitatu. Ni watoto 100 kwa mwaka na takribani Sh milioni 400 kwa mwaka. Tunatarajia ushirikiano huu kuwa wa mafanikio na tunatumaini utaendelea hata katika siku zijazo,” amesema Suryaningrat.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI na Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo, Dkt. Peter Kisenge, amesema msaada huo una umuhimu mkubwa kwa sababu utagusa moja kwa moja maisha ya watoto wanaohitaji huduma za haraka za moyo, wakiwemo wanaohitaji upasuaji na taratibu maalumu za kuziba matundu ya moyo.

“Huu si msaada wa pesa tu. Huu ni msaada unaokwenda kuokoa maisha. Mmeenda kutimiza matumaini ya watoto ambao wanakwenda kujenga Taifa la Tanzania la kesho,” amesema Dkt. Kisenge.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Global Medicare, Abdulmalik Mollel, amesema magonjwa ya moyo yanaendelea kuwa changamoto kubwa, huku JKCI ikiwa imejijengea nafasi muhimu katika utoaji wa huduma za kibingwa za moyo kwa Watanzania pamoja na wagonjwa kutoka nchi nyingine za ukanda huu, ikiwemo Zambia, Malawi, Kenya na Uganda.

Mollel amesema uamuzi wa GGML kutoa mchango huo ni hatua kubwa katika kusaidia watoto wenye matatizo ya moyo na unadhihirisha namna sekta binafsi inaweza kushirikiana na taasisi za Serikali katika kuokoa maisha.



Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
JUMUIYA ya Khoja Shia Ithnasheri Mkoa wa Dar es Salaam, kupitia taasisi zake, imeanza kutoa huduma mbalimbali za afya na macho bure kwa wananchi katika Kambi ya siku tatu ya Mafunzo ya Imam Hussein (a.s), inayofanyika katika Viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam.

Kambi hiyo imeandaliwa ikiwa ni sehemu ya kumbukumbu ya kifo cha mjukuu wa Mtume Muhammad (S.A.W), Imam Hussein (a.s), kilichotokea Karbala nchini Iraq zaidi ya miaka 1,400 iliyopita.

Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo Mkoa wa Dar es Salaam, Alhaji Mohammed Razzadewji, amesema maisha na mafundisho ya Imam Hussein yanasisitiza kujitolea kwa ajili ya jamii bila kubagua watu kwa misingi ya dini, kabila au jinsia.

Amesema Imam Hussein (a.s) alijitoa katika kuupigania umma wa babu yake, Mtume Muhammad (S.A.W), jambo ambalo linapaswa kuwa mfano wa kuigwa katika jamii.

Katika kambi hiyo, wananchi wamepatiwa huduma mbalimbali za afya, zikiwemo upimaji wa macho, shinikizo la damu, kisukari, saratani ya shingo ya kizazi na saratani ya matiti kwa wanawake, pamoja na uchunguzi wa tezi dume kwa wanaume.

Huduma nyingine zilizotolewa ni elimu kuhusu afya ya akili na uchangiaji wa damu salama, huku wananchi wakipata fursa ya kupata elimu kuhusu umuhimu wa kufahamu hali zao za kiafya.

Akizungumzia kambi hiyo, Alhaj Mohammedraza Dewji amesema kujitolea kwa ajili ya jamii ni sehemu ya misingi inayopaswa kuishi nayo kila mwanadamu, akirejea mfano wa Imam Hussein ambaye, kwa mujibu wa mafundisho hayo, alijitoa kwa ajili ya kulinda kizazi cha babu yake.

Amesema mwamko wa wananchi katika kambi hiyo umeongezeka ikilinganishwa na miaka iliyopita, ambapo kwa siku kambi hiyo ina uwezo wa kuhudumia hadi wagonjwa 2,000.

“Katika kambi ya safari hii kulikuwa na utofauti na mwaka jana. Wagonjwa wote waliokutwa na changamoto ya mtoto wa jicho walipelekwa moja kwa moja katika moja ya hospitali zetu, Medwell iliyopo Kibaha, Mkoa wa Pwani, na kwa wengine walipangiwa siku ya kwenda kupata matibabu katika hospitali zetu za Medwell na KSIJ Charitable Eye Centre iliyopo Temeke,” alisema Mohammedraza.

Amesema idadi kubwa ya wananchi waliojitokeza kupata huduma ni ishara ya mwamko mkubwa wa jamii kuhusu afya, huku akibainisha kuwa baadhi ya wananchi waligundulika kuwa na matatizo mbalimbali ambayo hawakuwa wakiyafahamu.

Kwa mujibu wa Mohammedraza, baadhi ya wananchi waligundulika kuwa na mtoto wa jicho, wengine uono hafifu na kupewa miwani, huku wengine wakipewa dawa za kutibu matatizo ya macho. Pia, wananchi walifanyiwa vipimo vya magonjwa yasiyoambukiza, ikiwemo shinikizo la damu.

Amesema Jumuiya hiyo ilishirikiana na Hospitali ya Taifa Muhimbili kupitia Kitengo cha Damu Salama pamoja na Taasisi ya Saratani Ocean Road katika kutoa huduma za uchunguzi wa saratani ya matiti na shingo ya kizazi kwa wanawake.

Amesisitiza umuhimu wa wananchi kujenga utamaduni wa kuchangia damu salama, akisema damu hiyo inahitajika katika hospitali mbalimbali, hususani kwa wanawake wajawazito na waathirika wa ajali.

Kwa upande wake, Mkuu wa Madaktari katika Kambi hiyo ya Afya na Macho, Dkt. Noushad Bandali, amesema uchangiaji wa damu ni huduma ya kujitolea ambayo inapaswa kuwa sehemu ya utamaduni wa kila mtu mwenye sifa ya kuchangia damu.

Dkt. Bandali amesema mahitaji ya damu katika hospitali ni makubwa, hivyo wananchi wanapaswa kujitokeza mara kwa mara kuchangia damu ili kusaidia kuokoa maisha ya wagonjwa.

Aidha, amesema kambi hiyo imetoa elimu kuhusu afya ya akili, eneo ambalo amesema bado halipatiwi uzito unaostahili katika jamii licha ya kuongezeka kwa changamoto zinazohusiana na afya ya akili, ikiwemo msongo wa mawazo.

Mmoja wa wanufaika wa kambi hiyo, Mariam Akida, mkazi wa Mbagala jijini Dar es Salaam, amesema amefaidika kwa kupata matibabu ya mtoto wa jicho baada ya kukabiliwa na tatizo la uono hafifu kwa muda mrefu bila kujua chanzo chake.

Amesema utaratibu uliowekwa na waandaaji wa kambi hiyo umekuwa mzuri kwa kuwa wananchi wamekuwa wakielekezwa katika maeneo mbalimbali ya huduma, hivyo kupunguza muda wa kusubiri.

Kwa upande wake, Mratibu wa Kambi hiyo kutoka Jumuiya ya Khoja Shia Ithnasheri Mkoa wa Dar es Salaam, Jahmeed Kassam, amesema wananchi wote watakaofika katika kambi hiyo ya siku tatu watahudumiwa na timu ya wawezeshaji na wataalamu wapatao 500 waliopo katika viwanja hivyo.

Kambi hiyo imehudhuriwa pia na viongozi mbalimbali wa dini, Serikali na siasa, huku wananchi wa maeneo mbalimbali ya Dar es Salaam wakijitokeza kwa wingi kupata huduma za afya na kushiriki katika mafunzo kuhusu maisha na mafundisho ya Imam Hussein (a.s).

 



Na Mwandishi Wetu - Zanzibar

Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL) limeendelea kuunga mkono juhudi za Serikali za kujenga mazingira wezeshi kwa uchumi wa kidijitali Zanzibar kwa kuwezesha huduma ya intaneti katika mradi wa makazi wa Amani Residency, uliopo Kizimkazi, Mkoa wa Kusini Unguja, kupitia huduma yake ya Faiba Mlangoni Kwako.

Mradi huo wa kisasa wa makazi ulizinduliwa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, ukiwa ni sehemu ya uwekezaji unaolenga kuongeza fursa za makazi bora, biashara na utalii pamoja na kuchochea shughuli za kiuchumi Zanzibar.

Akizungumza kuhusu uwezeshaji huo, Meneja wa TTCL Zanzibar, Bi. Nasra Mugheiry, alisema TTCL imeweka mazingira ya mawasiliano ya kisasa katika Amani Residency ili kuwawezesha wakazi kupata huduma ya intaneti karibu na makazi yao na kutumia fursa mbalimbali zinazotokana na uchumi wa kidijitali.

“TTCL kupitia huduma ya Faiba Mlangoni Kwako imeweka mazingira wezeshi ya mawasiliano katika Amani Residency, kwa lengo la kuwawezesha wakazi kutumia intaneti katika shughuli zao za kila siku, ikiwemo kazi, biashara, elimu, mawasiliano na huduma mbalimbali za kidijitali. Tunataka kuhakikisha kwamba makazi ya kisasa yanaendana na mahitaji ya kisasa ya mawasiliano,” alisema Bi. Mugheiry.

Huduma hiyo inatarajiwa kuongeza thamani ya mradi huo kwa kuwawezesha wakazi kufanya shughuli mbalimbali kwa urahisi wakiwa majumbani. Kwa wakazi wanaofanya kazi kwa njia ya mtandao, wafanyabiashara, wanafunzi na familia, upatikanaji wa intaneti ya nyumbani utarahisisha matumizi ya mikutano ya mtandaoni, kujifunza, kufanya biashara kupitia majukwaa ya kidijitali, mawasiliano pamoja na huduma za Serikali mtandao.

Amani Residency, unaojengwa katika eneo la ekari 11, una jumla ya nyumba 82, zikiwemo villa 18 na apartment 64, pamoja na huduma mbalimbali za burudani na mapumziko. Uwepo wa huduma ya Faiba Mlangoni Kwako unaifanya miundombinu ya mawasiliano kuwa sehemu muhimu ya mazingira ya makazi hayo, sambamba na mahitaji ya maisha ya kisasa.

Kwa upande wa biashara, intaneti inayopatikana katika makazi inaweza kuwapa wakazi fursa ya kuendesha shughuli zao za kiuchumi kwa kutumia teknolojia, ikiwemo biashara za mtandaoni, masoko ya kidijitali, huduma za kifedha na mawasiliano ya kibiashara. Hali hiyo inaendana na juhudi za TTCL za kuchochea matumizi ya teknolojia na kuunganisha wananchi na fursa za uchumi wa kidijitali.

Aidha, uwezeshaji huo unaimarisha dhamira ya TTCL ya kusogeza huduma za mawasiliano kwa wananchi katika maeneo wanayoishi na kufanya shughuli zao, kwa kuzingatia kwamba intaneti imekuwa sehemu muhimu ya maisha ya kila siku na kichocheo cha maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Kwa TTCL, kuwezesha Amani Residency kwa huduma ya Faiba Mlangoni Kwako ni zaidi ya kuunganisha makazi na intaneti; ni hatua ya kujenga mazingira ambayo yanawawezesha wananchi kuishi, kufanya kazi, kujifunza, kuwasiliana na kufanya biashara kwa kutumia teknolojia, sambamba na juhudi za taifa za kujenga uchumi unaotegemea zaidi huduma na fursa za kidijitali.






Wananchi wa Mkoa wa Tanga na mikoa jirani wanahamasishwa kushiriki katika Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ubunifu na Ujuzi, itakayofanyika kuanzia tarehe 15 - 24 Agosti 2026 katika viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara, jijini Tanga, ili kujifunza, kubadilishana maarifa na kutumia fursa mbalimbali za elimu, ujuzi na ubunifu.

Akizungumza Agosti 14, 2026, Katibu Tawala wa Mkoa wa Tanga, Rashid Kassim Mchata, amesema maonyesho hayo yatashirikisha taasisi zaidi ya 300 pamoja na wadau wa sekta ya elimu, sayansi na teknolojia. Aidha, kutakuwa na mashindano ya ubunifu na ujuzi katika fani mbalimbali ikiwemo ushonaji, ususi, umeme na mengineyo, ambapo washindi wa kitaifa watapata nafasi ya kushiriki mashindano ya kimataifa.

Mchata ameongeza kuwa wadhamini mbalimbali wakiwemo mabenki wamejitokeza kudhamini miradi ya ubunifu na kuunga mkono wajasiriamali chipukizi.

Kwa upande wake, Prof. Ladislaus Mnyone, Mkurugenzi wa Idara ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu, alisema lengo kuu la wiki hiyo ni kuwaleta pamoja wadau kujadili na kuweka mikakati ya pamoja kuhusu elimu, ujuzi na ubunifu.

Amebainisha kuwa matukio makuu yatakuwa ni maonesho ya teknolojia yanayoonyesha mchango wa sayansi katika sekta mbalimbali, pamoja na kongamano la elimu na ubunifu litakalojadili utekelezaji wa Dira 2050.

Prof. Mnyone amefafanua kuwa kongamano hilo litaangazia nyenzo tano kuu: utafiti na maendeleo, sayansi na ubunifu, teknolojia za kidijitali, nishati, na usafirishaji funganishi.

Kupitia mijadala na maonesho hayo, Wizara inalenga kufanikisha malengo ya taifa ikiwemo kufikia uchumi wa dola trilioni 1 ifikapo mwaka 2050, kipato cha wastani cha mtu mmoja kati ya Dola za Marekani 7,000 - 12,000, na ajira zenye staha kwa angalau asilimia 50 ya Watanzania.


Top News