Na Janeth Raphael - MichuziTv
Shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo (FAO) limezindua mfumo wa kidijitali wa TANFISH, unaolenga kuwaunganisha wavuvi, wasindikaji wa samaki na wanunuzi ili kurahisisha biashara ya mazao ya uvuvi na kuwafungulia wazalishaji masoko mapana zaidi ndani na nje ya maeneo yao
Akizungumza katika hafla hiyo iliyofanyika Dodoma, Mtaalamu wa Kimataifa wa Mnyororo wa thamani wa Uvuvi na Ufugaji wa Viumbe Maji wa FAO, Hasheem Muumin, amesema TANFISH inawawezesha wavuvi na wasindikaji kujisajili kwenye mfumo, kuweka picha na taarifa za bidhaa zao na kuwasiliana moja kwa moja na wanunuzi kutoka maeneo mbalimbali nchini.
Amesema mfumo huo unahudumia aina mbalimbali za bidhaa za uvuvi, zikiwemo samaki wabichi, waliokaushwa na waliogandishwa kutoka kwenye maji ya bahari, maziwa pamoja na shughuli za ufugaji wa samaki.
Kwa mujibu wa Muumin, TANFISH pia imejengwa kwa kuimarisha usalama wa miamala, ikiwemo kulinda malipo ya wanunuzi, huku ikiwawezesha wavuvi na wasindikaji kupata masoko makubwa na yenye uhakika zaidi.
“TANFISH inalinda malipo ya wanunuzi huku ikiwawezesha wavuvi na wasindikaji kupata masoko makubwa na yenye uhakika zaidi,” amesema Dkt. Muumin.
Amesema hadi sasa FAO imewapatia mafunzo zaidi ya wavuvi, wasindikaji na wadau wengine 500, ambao tayari wamesajiliwa katika mfumo huo.
Aidha, zaidi ya tani mbili za samaki tayari zimeuzwa kupitia TANFISH, huku Dodoma ikiwa miongoni mwa masoko makubwa yaliyofikiwa na mfumo huo pamoja na maeneo mengine nchini.
Muumin amesema TANFISH ilianza kwa kulenga zaidi jamii zinazozunguka Ziwa Tanganyika, lakini sasa imepanuka na kuwajumuisha wasindikaji na wafanyabiashara kutoka Ziwa Victoria pamoja na maeneo ya pwani ya Tanzania, hatua inayolenga kujenga soko la kidijitali la bidhaa za uvuvi linalounganisha maeneo mbalimbali nchini.
Mfumo huo unapatikana kupitia vifaa vya Android na Apple, hivyo kuwawezesha watumiaji kuupata na kufanya biashara kwa urahisi zaidi.
Ili kuhakikisha ubora wa bidhaa na kulinda uaminifu wa watumiaji, wauzaji wanatakiwa kuzingatia matakwa yote ya kisheria na kanuni za Serikali, ikiwemo kuwa na nyaraka halali za biashara.
Kwa upande wa wanunuzi, wanatakiwa kutoa taarifa sahihi za mahali bidhaa zinapopaswa kufikishwa ili kurahisisha usafirishaji na kuhakikisha samaki wanafika kwa usalama na kwa wakati.
Uzinduzi wa TANFISH ni sehemu ya juhudi za FAO za kutumia teknolojia na mifumo ya kidijitali kuimarisha minyororo ya thamani ya kilimo na uvuvi, kuongeza fursa za masoko na kuchochea ongezeko la kipato kwa wazalishaji nchini.