Na Mwandishi Wetu

MTAALAMU katika sekta ya nishati, hususan mafuta nchini, Dkt. Sajad Habib Rai, ameteuliwa kuwa mjumbe na mmoja wa wazungumzaji katika Mkutano wa World CEO Summit 2026 Africa, unaotarajiwa kufanyika Novemba 26 na 27, 2026, jijini Dar es Salaam.

Mkutano huo wa kimkakati unaolenga kujadili masuala ya uwekezaji, biashara na maendeleo ya kiuchumi, unatarajiwa kuwakutanisha zaidi ya Wakurugenzi Wakuu (CEOs) 1,000, wawekezaji, watunga sera na viongozi wa sekta mbalimbali kutoka zaidi ya nchi 50.

Dkt. Sajad, ambaye ni Meneja Mkazi wa Mansoor Industries Limited, anatarajiwa kuzungumzia uzoefu wake katika masuala ya maendeleo ya viwanda, nishati, uwekezaji, uendelevu na ushirikiano wa kimkakati kwa ajili ya kukuza uchumi wa Afrika.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na waandaaji wa mkutano huo, Dkt. Rai atashirikisha mitazamo na uzoefu kuhusu maendeleo ya viwanda, nishati, uendelevu na uwekezaji, pamoja na ushirikiano wa kimkakati unaohitajika kuimarisha uwezo wa uzalishaji barani Afrika na kuharakisha mabadiliko ya kiuchumi.

Akizungumzia ushiriki wake katika mkutano huo, Dkt. Sajad, ambaye kwa muda mrefu amekuwa mshauri katika sekta ya nishati, hususan mafuta, amesema anatarajia kutumia fursa hiyo kushirikisha uzoefu wake na kujifunza kutoka kwa wazungumzaji na washiriki wengine.

“Nimepokea mwaliko wa mkutano huo kwa furaha kubwa. Lengo ni kuchangia uchumi wa nchi yetu na kuhamasisha uwekezaji. Hivyo, nami kama mzalendo wa nchi hii nitajifunza mengi, lakini pia nitatoa uzoefu wangu ili kwa pamoja tuweze kuijenga Tanzania na Afrika inayojitegemea kiuchumi,” amesema Dkt. Sajad.

Amesema ushiriki wake katika mkutano huo ni fursa muhimu ya kuitangaza Tanzania katika jukwaa la kimataifa, hususan katika maeneo ya uwekezaji, nishati na maendeleo ya viwanda.

World CEO Summit Africa ni mkutano unaowakutanisha viongozi wa kampuni, Serikali na wawekezaji kwa lengo la kujadili namna ya kukuza biashara na uchumi wa Afrika.

Mkutano wa mwaka huu una kaulimbiu isemayo “Uniting Leadership, Capital and Policy for Africa’s Transformation”, inayolenga kuunganisha uongozi, mitaji na sera kwa ajili ya kuharakisha mabadiliko ya Afrika.

Miongoni mwa masuala yanayotarajiwa kujadiliwa katika mkutano huo ni upatikanaji wa mitaji, maendeleo ya viwanda na biashara, uongozi na sera za kiuchumi, teknolojia na ubunifu wa Akili Unde (AI), nishati na miundombinu, pamoja na kilimo na usalama wa chakula.

Masuala mengine ni huduma za kifedha, afya na mali isiyohamishika, uendelevu na ukuaji wa biashara, pamoja na ushirikiano wa kimkakati, ubia na upanuzi wa masoko.



Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

MKUU wa Wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo, amesema mtu atakayebainika kutupa taka hovyo jijini Dar es Salaam atatozwa faini ya Shilingi 300,000 hadi milioni moja au kuhukumiwa kifungo cha miezi 12 hadi 24, kwa mujibu wa Kifungu cha 41 cha Sheria Ndogo ya Afya, Usafi na Usimamizi wa Mazingira ya Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam ya Mwaka 2024 (GN Na. 1011).

Akizungumza jana, Septemba 19, 2026, baada ya kuhitimisha zoezi la usafi wa mazingira jijini, Mpogolo amesema sheria hiyo imeanza kutekelezwa kikamilifu kwa lengo la kuhakikisha Dar es Salaam inakuwa safi, salama na yenye mazingira bora.

“Atakayekutwa anatupa uchafu hovyo atachukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria. Adhabu ni faini ya kuanzia Shilingi laki tatu hadi milioni moja au kifungo cha miezi 12 hadi 24. Kila mmoja anatakiwa kutambua wajibu wake na kuacha mara moja tabia ya kutupa uchafu hovyo,” amesema.

Amesema Serikali itaendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa usafi wa mazingira, lakini hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi ya watakaokiuka sheria kwa kutupa taka hovyo, kutiririsha maji au kufanya vitendo vingine vinavyohatarisha usafi na mazingira.

Mpogolo amesema utekelezaji wa sheria hiyo haulengi kutoa adhabu pekee, bali kujenga nidhamu, uwajibikaji na utamaduni wa usafi miongoni mwa wananchi.

Amesema Halmashauri itaendelea kuweka maeneo na vifaa vya kuhifadhia taka pamoja na kuhamasisha utenganishaji wa taka kulingana na aina zake ili kurahisisha ukusanyaji na utunzaji wa mazingira.

Ili kuimarisha ufuatiliaji, Mpogolo amesema Jiji limejipanga kuajiri vijana waliomaliza mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) na kuwapatia vyombo vya usafiri kwa ajili ya kusimamia usafi katika mitaa mbalimbali.

“Tutakwenda mtaa kwa mtaa. Hatutaki kuona mtu anatupa taka popote anapotaka. Tutakuwa na mfumo wa ufuatiliaji wa karibu ili kuhakikisha sheria inatekelezwa ipasavyo,” amesema.

Aidha, amesema barabara zote muhimu za Jiji, maarufu kama Smart Roads, zitasimamiwa kikamilifu ili zibaki safi, zipandwe miti rafiki na salama na ziendelee kulipamba Jiji.

Amesema biashara katika barabara hizo hazitaruhusiwa bila kibali cha Mkurugenzi wa Jiji, huku wafanyabiashara wakitakiwa kufanya shughuli zao katika maeneo yaliyopangwa.

Amesema hatua hiyo inalenga kupunguza msongamano, kuimarisha usalama wa watumiaji wa barabara na kuhakikisha Jiji la Dar es Salaam linakuwa na mazingira safi na yanayovutia.


Na Mwamvua Mwinyi, Pwani

WAKALA wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) Mkoa wa Pwani, umeanza kutekeleza agizo la Serikali la kukagua miundombinu ya barabara na madaraja hatarishi na kuyafanyia matengenezo, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya kukabiliana na athari zinazoweza kusababishwa na mvua kubwa za El Niño zinazotarajiwa.

Katika utekelezaji huo, TARURA Pwani imebaini jumla ya maeneo 221 yenye hatari ya mafuriko, ambapo maeneo 138 yako katika kiwango cha juu cha hatari na 83 katika kiwango cha kati.

Meneja wa TARURA Mkoa wa Pwani, Ibrahim Kibasa, amesema wakala huo unaendelea kufanya tathmini ya maeneo hayo kwa kushirikisha wataalamu, huku hatua za awali zikichukuliwa ikiwemo kusafisha mifereji, makaravati na njia za kupitisha maji ili kupunguza athari kwa wananchi na miundombinu ya barabara.

Amesema tathmini na udhibiti wa mtiririko wa maji unaendelea katika maeneo ya Chumbi, Muhoro na Ikwiriri wilayani Rufiji, huku maeneo mengine yakiendelea kufanyiwa uchambuzi kulingana na kiwango cha hatari kilichobainika.

Kibasa amesema TARURA pia imetumia vikundi maalumu kufanya usafi wa mifereji na makaravati pamoja na kuzibua maeneo yanayoweza kuzuia mtiririko wa maji, ambapo kwa sasa vikundi 23 vinafanya kazi wilayani Rufiji.

Amesema mpango huo ni kuongeza vikundi hivyo katika halmashauri nyingine, ikiwemo Kibaha, Kisarawe na Bagamoyo, huku maeneo yanayoendelea kufanyiwa tathmini yakijumuisha Delta ya Rufiji, Kibiti na Mkuranga.

“Tunaendelea kuainisha maeneo hatarishi ambayo yamekuwa yakiripotiwa na kutafuta njia mbadala za kukabiliana na changamoto hizo, pamoja na kutoa elimu ya usalama wa matumizi ya barabara katika maeneo hayo,” amesema Kibasa.

Ameongeza kuwa TARURA itashirikiana na Jeshi la Polisi na mamlaka nyingine kutoa tahadhari kuhusu matumizi salama ya barabara katika maeneo yenye hatari, huku timu za mwitikio wa dharura zikiwa zimeundwa katika ngazi ya Mkoa, Wilaya na TARURA Taifa.

Kwa mujibu wa Kibasa, timu hizo zitashirikiana na timu za maafa, Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, TANROADS, TANESCO, mamlaka za maji, Jeshi la Polisi, waandishi wa habari pamoja na wakandarasi wanaotekeleza miradi ya barabara katika kukabiliana na dharura endapo zitatokea.

Amesema TARURA Pwani tayari imejiandaa kwa vifaa vya dharura, ikiwemo makaravati ya plastiki 30, vikapu 60 vya kuweka mawe pamoja na vifaa vingine vitakavyotumika katika maeneo yatakayokumbwa na changamoto.

Kwa upande wake, Mhandisi wa TARURA Wilaya ya Kibaha, David Kakole, amesema wanaendelea na matengenezo ya miundombinu ya barabara, ikiwemo barabara ya kimkakati inayoelekea Kituo cha Reli ya Kisasa (SGR) Soga, pamoja na kurekebisha maeneo yenye changamoto ili kuboresha usafiri na kurahisisha shughuli za wananchi.

Naye Meneja wa TARURA Wilaya ya Bagamoyo, Bupe Angetile, amesema wanaendelea kutekeleza maelekezo ya Serikali, Wizara na Mkoa katika kujiandaa na tahadhari zinazohusiana na mvua za El Niño.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Stanslaus Nyongo, amesema Serikali imejipanga kukabiliana na athari zinazoweza kujitokeza, huku akisisitiza TARURA na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) kukagua madaraja yote hatarishi na kuyafanyia marekebisho.

Amewataka wakandarasi wanaotekeleza miradi ya ujenzi na ukarabati wa madaraja kuhakikisha wanakamilisha kazi kwa wakati ili kuondoa hatari kwa wananchi na kuhakikisha miundombinu hiyo inakuwa salama wakati wa mvua kubwa.





MAKAMISHNA Wasaidizi Waandamizi wa Uhifadhi wanawake kutoka Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) wapo nchini Indonesia kushiriki mkutano wa mtandao wa wanawake maafisa waandamizi wa Polisi na vyombo vingine vya usalama unaofanyika nchini humo.

Makamishna hao wanaongozwa na Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Rasilimali Watu na Utawala, Salma Chisonga, ambapo wanatarajiwa kushiriki katika majadiliano na kubadilishana uzoefu kuhusu masuala ya ulinzi, uhifadhi, utalii na maendeleo ya jamii.

Mkutano huo wa siku tano umewakutanisha wanawake kutoka vyombo mbalimbali vya usalama kutoka nchi tofauti duniani kwa lengo la kujadili fursa na changamoto zinazowakabili wanawake katika vyombo vya usalama pamoja na taasisi zinazolinda rasilimali za nchi.

Aidha, ushiriki wa makamishna hao unatarajiwa kutoa fursa kwa Tanzania kubadilishana uzoefu na mataifa mengine kuhusu namna ya kuimarisha ushiriki wa wanawake katika ulinzi, uhifadhi wa rasilimali na usimamizi wa maeneo ya utalii.

Mkutano huo pia unalenga kuimarisha ushirikiano na mitandao ya wanawake katika vyombo vya usalama duniani, huku ukitoa nafasi ya kujifunza mbinu na uzoefu mbalimbali katika kukabiliana na changamoto za kiusalama na uhifadhi.


ZANZIBAR

NAIBU Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar, Ndugu Abdi Mahamoud Abdi, amepongeza hatua za utekelezaji wa mradi wa Bandari Jumuishi ya Mangapwani, akisema kukamilika kwake kutachochea ukuaji wa uchumi wa Zanzibar na Taifa kwa ujumla.

Ndugu Abdi ameyasema hayo leo, Septemba 20, 2026, wakati akiendelea na ziara yake katika Jimbo la Bumbwini, ambapo ametembelea na kukagua maendeleo ya ujenzi wa Bandari ya Mafuta na Gesi Asilia Zanzibar inayojengwa Mangapwani.

Amesema CCM imeridhishwa na hatua zinazochukuliwa katika utekelezaji wa mradi huo, ambao unatarajiwa kuwa na mchango mkubwa katika kukuza shughuli za kiuchumi, kuongeza fursa za ajira na kuimarisha miundombinu ya usafirishaji na biashara Zanzibar.

Aidha, amempongeza Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Ali Mwinyi, kwa kuendelea kutekeleza ahadi za Serikali kwa vitendo, ikiwemo ujenzi wa bandari hiyo ya kisasa.

Ndugu Abdi amesema ujenzi wa Bandari ya Mangapwani utasaidia kuongeza fursa za ajira kwa wananchi, hususan katika maeneo ya Kaskazini Unguja, pamoja na kuchochea shughuli mbalimbali za kiuchumi zinazozunguka bandari hiyo.

Amesema bandari hiyo pia itakuwa na nafasi muhimu katika uhifadhi wa mafuta, hatua ambayo itasaidia kupunguza changamoto za upatikanaji wa bidhaa hiyo na kuimarisha upatikanaji wake wakati wa mabadiliko ya bei katika masoko mbalimbali.

“Ujenzi wa Bandari ya Mangapwani ni miongoni mwa hatua zinazoonesha namna Zanzibar inavyoendelea kufunguka katika maendeleo endelevu kupitia sekta ya bahari na uchumi wa buluu,” amesema.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Shirika la Bandari Zanzibar, Akif Ali Khamis, amesema mradi huo unakadiriwa kugharimu Dola za Marekani milioni 30 hadi kukamilika kwake.

Naye Mkandarasi wa Mradi wa Mafuta na Gesi Asilia Mangapwani, Salum Udi, amesema kutokana na kina cha maji katika eneo hilo, bandari hiyo itakuwa na uwezo wa kuhudumia meli kubwa zenye uwezo wa kubeba hadi makontena 20,000.

Amesema ujenzi wa bandari hiyo pia utahusisha miundombinu mbalimbali ya kisasa, ikiwemo bandari ya mafuta na gesi asilia, miundombinu ya kijamii, upatikanaji wa maji safi na salama, viwanja vya michezo pamoja na maeneo ya mapumziko kwa wananchi.










 

NAIBU Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar, Ndugu Abdi Mahamoud Abdi, amewapongeza viongozi wa Jimbo la Donge kwa juhudi za kutafuta wadau na wahisani wanaosaidia utekelezaji wa miradi ya elimu na malezi ya watoto.

Ndugu Abdi ameyasema hayo baada ya kutembelea na kukagua miradi ya skuli pamoja na kituo cha kulelea watoto yatima katika Jimbo la Donge, ambapo amesema jitihada hizo zina mchango mkubwa katika kuboresha huduma za elimu na malezi.

Amesema kituo hicho ni miongoni mwa njia muhimu za kuhakikisha watoto wanapata malezi bora, elimu na mazingira salama yatakayowasaidia kukua katika misingi ya maadili na kuwa vijana wema wenye elimu na ujuzi wa kukabiliana na changamoto za maisha.

“Ndugu Abdi amesema CCM inapongeza jitihada zinazofanywa na viongozi wa Jimbo la Donge katika kuibua na kuendeleza miradi inayolenga kuchochea maendeleo ya elimu pamoja na kuboresha mazingira ya malezi ya watoto nchini.”

Aidha, amesema ushirikiano kati ya viongozi na wadau mbalimbali ni muhimu katika kuhakikisha miradi hiyo inakamilika na kutoa huduma zinazokusudiwa kwa jamii.

Miradi hiyo inajengwa kwa ufadhili wa Taasisi ya Al-Attah Charitable Organization, ambapo inatarajiwa kuwa na mchango mkubwa katika kuhakikisha watoto wanapata malezi bora, elimu na mazingira salama kwa maendeleo yao.









MOSHI

MKUU wa Mkoa wa Kilimanjaro, Nurdin Babu, amewaagiza wafanyabiashara wanaopanga bidhaa zao chini katika barabara zinazozunguka Soko la Mbuyuni, Manispaa ya Moshi, kuondoka katika maeneo hayo na kuhamia ndani ya soko hilo ili kuepuka milipuko ya magonjwa na uchafuzi wa mazingira.

Babu alitoa agizo hilo jana wakati akishiriki zoezi la usafi katika Soko la Mbuyuni, ambapo alisema barabara zimejengwa kwa ajili ya kupitisha magari na wananchi, hivyo hazipaswi kutumika kama maeneo ya kufanyia biashara.

Alisema wafanyabiashara wanaofanyia biashara pembezoni mwa barabara wanapaswa kufika kwa viongozi wa soko hilo ili kupangiwa maeneo rasmi ya kufanyia biashara, kabla Serikali haijachukua hatua za kuwaondoa katika maeneo hayo.

“Niwaombe muanze kuondoka wenyewe mapema, tusije tukaja kuwaondoa sisi mkasema tunawaonea. Serikali imetumia fedha nyingi kujenga masoko haya, hivyo ni wajibu wenu kufanya biashara ndani ya masoko haya ambayo yamewekewa miundombinu rafiki ya kuwahudumia,” alisema Babu.

Mkuu huyo wa mkoa alisema wafanyabiashara hao wakijipanga na kufanya shughuli zao ndani ya soko, wateja wataendelea kuwafuata huko kwa ajili ya kununua bidhaa.

Alisisitiza kuwa agizo hilo linapaswa kutekelezwa bila shuruti, akiwataka wafanyabiashara kuzingatia taratibu na sheria zilizowekwa kwa ajili ya kuhakikisha usalama, usafi na ustawi wa wananchi.







Mbuzi wa Benki ya NMB, ‘NMB the GOAT’, ameibuka mshindi katika mbio za ‘NMB unGOATable Race’ zilizofanyika Septemba 19, 2026, akimshinda mbuzi wa Bowman katika mashindano Goat Races yanayolenga kuchangisha Sh200 milioni kwa ajili ya kusaidia elimu ya juu kwa vijana 150. NMB imeshiriki kwa mara ya kwanza kama mmoja wa wadhamini wakuu wa mashindano hayo.

Akizungumza baada ya ushindi huo, Mkuu wa Idara ya Huduma za Kibenki kwa Wateja Maalumu wa NMB, Getrude Mallya, alisema ushindi wa mbuzi huyo umefanya ushiriki wa kwanza wa benki katika mashindano hayo kuwa wa kipekee. Alisema NMB inajivunia kuunga mkono tukio linalounganisha burudani na uchangishaji wa fedha kwa ajili ya kuwasaidia vijana wenye changamoto za kifedha kuendelea na masomo.

"Zaidi ya furaha ya ushindi, ushiriki wetu katika mashindano haya unaakisi dhamira ya Benki ya NMB ya kuunga mkono jitihada zinazofungua fursa kwa vijana wa Kitanzania. Mashindano haya yanatuunganisha kwa lengo muhimu la kuchangisha fedha kusaidia elimu," alisema Mallya.

Kwa mujibu wa Rais wa Rotary Club ya Dar es Salaam Oysterbay, Paul Muhato, wanafunzi 350 wamewezeshwa kuendelea na masomo tangu klabu hiyo ilipoanza kusimamia rasmi mashindano hayo mwaka 2018. Mashindano ya mwaka huu yanalenga kuongeza idadi hiyo kwa kuwawezesha wanafunzi wengine 150 kupata elimu ya juu mwaka ujao.













Na Victor Masangu, Bagamoyo

MBUNGE wa Jimbo la Bagamoyo, Mhe. CPA Subira Khamisi Mgalu, ameipongeza Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Bagamoyo kwa ubunifu na mipango madhubuti inayolenga kuongeza ufanisi katika ukusanyaji wa mapato.

Mhe. Mgalu aliyasema hayo wakati wa ziara yake katika Ofisi za TRA Bagamoyo, ambapo alipata fursa ya kukutana na kufanya mazungumzo na Meneja wa TRA Bagamoyo, Mariam Omari.

Katika mazungumzo hayo, walijadili masuala mbalimbali yanayohusu ongezeko la mapato, ukusanyaji wa kodi, mikakati ya kuvuka malengo ya ukusanyaji pamoja na umuhimu wa kuendelea kuwaelimisha na kuwahamasisha wananchi kuhusu ulipaji wa kodi.

Mhe. Mgalu ameipongeza TRA Bagamoyo kwa kazi inayofanyika katika kuhakikisha ukusanyaji wa mapato unaendelea kuimarika, akisema hatua hizo ni muhimu katika kuchochea maendeleo ya Taifa na Jimbo la Bagamoyo.

Aidha, ameahidi kuendelea kutoa ushirikiano kwa TRA na kuhamasisha wananchi kupitia mikutano yake mbalimbali kuhusu umuhimu wa kulipa kodi kwa wakati ili kuwezesha Serikali kutekeleza miradi ya maendeleo.

Mbunge huyo pia amempongeza Meneja wa TRA Bagamoyo, Mariam Omari, kwa moyo wa kujitolea na kushirikiana na jamii, hususan katika kuchangia uboreshaji wa miundombinu katika Shule ya Msingi Ukuni.

Amesema ushiriki wa taasisi na watendaji katika shughuli za kijamii ni mfano mzuri wa ushirikiano kati ya Serikali, taasisi na wananchi, hivyo unapaswa kuungwa mkono na kuendelezwa.

Mhe. Mgalu ameahidi kuwa balozi wa kuhamasisha ushirikiano kati ya wananchi, taasisi na wadau mbalimbali katika kuhakikisha juhudi za maendeleo ya Bagamoyo zinaendelea kuimarika.

Amesisitiza kuwa ushirikiano kati ya viongozi, taasisi na wananchi ni muhimu katika kuongeza uelewa kuhusu ulipaji wa kodi, kuimarisha ukusanyaji wa mapato na kuchochea kasi ya maendeleo.




WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba ameondoka nchini leo (Jumamosi, Septemba 19, 2026) kwenda Roma, Italia kumwakilisha Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika Mkutano wa siku tatu wa Kimataifa wa Kujadili Afya Moja na Mifumo ya Chakula na Kilimo. 

Mkutano huo utakaofanyika katika Makao Makuu ya Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO), jijini Roma, Italia kuanzia Septemba 21–23, 2026 unalenga kuimarisha utekelezaji wa dhana ya Afya Moja (One Health) inayotambua uhusiano kati ya afya ya binadamu, wanyama, mimea na mazingira, kwa lengo la kuhakikisha mifumo endelevu ya chakula na kilimo

Mkutano huo utahusisha viongozi wa nchi na Serikali, wakiwemo Marais kati ya watano hadi saba, Mawaziri kati ya 30 hadi 50, pamoja na wawakilishi wa taasisi za kikanda na kimataifa, wadau wa maendeleo, sekta binafsi, taasisi za utafiti na mashirika ya kimataifa.

 Mambo muhimu yatakayojadiliwa katika mkutano huo ni Ujumuishaji wa dhana ya Afya Moja (One Health) katika sera na uwekezaji wa mifumo ya chakula na kilimo; na uimarishaji wa ushirikiano wa kisekta kati ya sekta za kilimo, mazingira, afya, fedha na mipango ya miji.

Mengine ni ukuzaji wa ubunifu, sayansi na maarifa ya ndani ili kuboresha uzuiaji wa vihatarishi, ufuatiliaji na usimamizi endelevu wa rasilimali na kuhamasisha uwekezaji na ushirikiano ili kutafsiri ahadi kuwa hatua madhubuti zenye matokeo yanayopimika.





Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Deogratius John Ndejembi, amezitaka Taasisi za Muungano kuimarisha ushirikiano, kubaini na kutumia fursa zilizopo pamoja na kushiriki kwa pamoja katika shughuli mbalimbali ndani na nje ya nchi kwa lengo la kuongeza tija na kuleta manufaa zaidi kwa Watanzania.

 Makamu wa Rais ametoa wito huo leo, Septemba 19, 2026 wakati akifungua kikao cha Wakuu wa Taasisi za Muungano kilichofanyika katika Ukumbi wa Golden Tulip, Zanzibar, na kuhudhuriwa na wakuu wa Taasisi 39 za Muungano.

Makamu wa Rais amewataka viongozi wa taasisi hizo kuelewa kwa kina wajibu wao katika kuwahudumia wananchi na kufanya kazi kwa mtazamo mmoja wa kujenga “nyumba moja”, huku maslahi ya Watanzania yakiwekwa mbele.

Amesema matarajio ya wananchi ni kuona Muungano na taasisi zake zikitoa matokeo yanayogusa maisha yao moja kwa moja, hususan katika kuboresha hali ya uchumi, afya, elimu na maeneo mengine muhimu ya kijamii.

 Amezihimiza taasisi hizo kuondoa vikwazo vinavyoweza kudhoofisha ushirikiano na badala yake kutumia fursa zilizopo katika pande zote mbili za Muungano ili kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao.

Aidha, Mhe. Ndejembi ameahidi kuwa Ofisi ya Makamu wa Rais itaendelea kuunga mkono jitihada za Taasisi za Muungano kwa kuratibu, kusimamia, kushauri na kuziwezesha kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi zaidi, kwa lengo la kuharakisha maendeleo na kuboresha huduma kwa wananchi.

 Akizungumza kabla ya kumkaribisha Makamu wa Rais, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni, amesema kikao hicho kinalenga kuimarisha ushirikiano kati ya taasisi za Muungano na Ofisi ya Makamu wa Rais; na kuongeza uelewa wa pamoja kuhusu masuala mbalimbali ya Muungano na majukumu yanayotekelezwa na taasisi hizo, sambamba na kuweka mwelekeo wa kuimarisha utendaji kazi na kuongeza ufanisi.

 Kikao hicho cha Wakuu wa Taasisi za Muungano ambacho pia kimehudhiriwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar, Mhe Hamza Hassan Juma, Makatibu Wakuu na Watendaji Wakuu wa Taasisi kinatoa  nafasi kwa viongozi hao kujadili namna ya kuimarisha uratibu, kubadilishana uzoefu na kuweka mikakati ya pamoja itakayoongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao kwa manufaa ya wananchi







Top News