Tanzania inatarajiwa kuwa mwenyeji wa Africa Tourism Private Sector Alliance (ATPSA) Tourism Roadshow Tanzania 2026, jukwaa litakalowakutanisha wafanyabiashara wa utalii, wanunuzi na wadau kutoka mataifa mbalimbali ya Afrika kwa ajili ya kukuza biashara na ushirikiano katika sekta hiyo.

Roadshow hiyo itafanyika Zanzibar Septemba 27, 2026, katika Hotel Verde Zanzibar, kabla ya kuhamia Arusha Septemba 30, 2026, katika Gran Meliá Arusha.

Tukio hilo linafanyika wakati Tanzania ikiendelea kuimarisha nafasi yake katika sekta ya utalii barani Afrika, baada ya kutambuliwa kuwa Africa’s Leading Destination 2026, huku Bodi ya Utalii Tanzania ikishinda tuzo ya Africa’s Leading Tourist Board 2026 kwa mwaka wa tano mfululizo.

Mkurugenzi wa Idara ya Utalii, Dr. Thereza Mugobi, amesema Roadshow hiyo ni fursa kwa Tanzania kutangaza vivutio vyake, lakini pia kushiriki katika kujenga soko la utalii la Afrika kwa Waafrika.

Kwa upande wake, Madam Devotha Mdachi, Mjumbe wa Bodi na Mwakilishi Rasmi wa Africa Tourism Partners (ATP) na Africa Tourism Private Sector Alliance (ATPSA) kwa ukanda wa Afrika Mashariki, amewataka wadau wa utalii nchini kutumia fursa hiyo kujenga masoko mapya na ushirikiano wa kibiashara.

Washiriki kutoka nchi mbalimbali zikiwemo Botswana, Ethiopia, Ghana, Kenya, Malawi, Uganda, Namibia, Nigeria, Rwanda na Afrika Kusini, pamoja na India na Belgium, wanatarajiwa kushiriki katika mikutano hiyo.

Msingi wa Roadshow utakuwa ni mikutano ya biashara kwa biashara (B2B), ambapo washiriki watatumia mfumo wa ATPSA B2B Appointment Platform kupanga mikutano na washirika wao wa biashara. Kila mshiriki atapata nafasi ya kufanya hadi mikutano 15 iliyopangwa kabla.

Kaulimbiu ya Roadshow hiyo ni “Meet. Connect. Trade. Grow Africa.”, ikiwa na lengo la kuimarisha biashara ya utalii, ushirikiano wa sekta binafsi na kukuza utalii wa ndani ya Afrika.

ATPSA inaeleza kuwa mustakabali wa utalii barani Afrika unahitaji nchi, biashara na watu kuunganishwa zaidi ili kujenga soko imara la utalii ndani ya bara.










Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimewapa jukumu makada wake 460 kutoka kanda tisa za kichama kusimamia maadili na Itikadi ya Chama, pamoja na kuchangia upatikanaji wa wanachama wapya katika wilaya mbalimbali nchini.

Makada hao wamepewa jukumu hilo kupitia mafunzo ya Itikadi, Uenezi na kuongeza wanachama wapya yanayoendelea katika Chuo cha UVCCM Ihemi, mkoani Iringa, kuanzia Septemba 15 hadi 21, 2026.

Badala ya mafunzo hayo kuishia darasani, CCM imewataka washiriki kuyageuza kuwa utekelezaji wa moja kwa moja katika maeneo yao kwa kuwafikia wanachama na wananchi, kutoa elimu sahihi kuhusu Chama na kushiriki katika ujenzi na uimarishaji wa CCM.

Akifungua mafunzo hayo, Makamu Mwenyekiti wa CCM Bara, Stephen Wasira, amesema makada hao wanapaswa kuwa sehemu ya mabadiliko yanayofanywa ndani ya Chama kwa kutumia maarifa wanayoyapata kupitia mafunzo hayo.

“Makada waliopata mafunzo haya wanapaswa kuyatumia kuwafikia wanachama ili kutoa elimu kwa usahihi,” amesema Wasira.

Amesema CCM ina historia ndefu na nafasi yake katika siasa za Tanzania inawataka makada kuelewa kwa kina misingi na Itikadi ya Chama na kuisimamia katika utekelezaji wa majukumu yao.

Wasira amesema jukumu la makada hao halipaswi kuishia katika kuongeza idadi ya wanachama pekee, bali linapaswa kwenda sambamba na kuhakikisha wanaojiunga na CCM wanaelewa misingi, Itikadi na wajibu wao ndani ya Chama.

Kwa upande wake, Katibu wa NEC, Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa CCM, Kenani Kihongosi, amesema makada hao hawakuchaguliwa kwa bahati, bali walipitia mchakato wa usajili na usaili uliofanyika katika kanda zote tisa za kichama kabla ya kuanza mafunzo.

“Awamu hii ni ya kwanza na makada 460 wamepata mafunzo. Kabla ya kuanza mafunzo, kila kanda ilifanya usajili na usaili wa washiriki,” amesema Kihongosi.

Amesema mpango huo unalenga kujenga wataalamu wa mafunzo katika kila wilaya, watakaokuwa na uwezo wa kufikisha elimu ya Chama hadi katika ngazi za chini.

“Kinachojengwa katika mafunzo haya ni utekelezaji wa mfano wa kitaifa unaolenga kujenga wataalamu wa mafunzo katika kila wilaya,” amesema.

Kihongosi amesema miongoni mwa malengo makubwa ya mpango huo ni kuhakikisha kila wilaya inachangia kupata wanachama wapya 500.

“Lengo ni kusajili wanachama wapya 500 kila wilaya nchini. Washiriki wanapaswa kubeba yale watakayofundishwa na kuyafikisha kwa wananchi ili kuhakikisha wanapata elimu wanayoitarajia na kujenga Chama,” amesema.

Nao washiriki wa mafunzo hayo wamesema jukumu walilopewa ni kubwa, kwa kuwa linawataka kutokaa na elimu waliyoipata, bali kuifikisha kwa wanachama na wananchi katika maeneo yao.

“Tunatakiwa kuhakikisha elimu hii haibaki kwetu. Tukirejea kwenye maeneo yetu, tunapaswa kuwafikia wanachama na kuwaeleza kwa usahihi yale tuliyojifunza,” amesema Noel Chilaga.

Mafunzo hayo yameandaliwa na Idara ya Itikadi, Uenezi na Mafunzo ya CCM Taifa.








Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Umma, Jaji Mstaafu Hamisa Kalombola, amewataka watumishi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) kuzingatia maadili ya utumishi wa umma, uadilifu, uzalendo na uwajibikaji katika kutekeleza majukumu yao kwa maslahi ya taifa.

Jaji Mstaafu Hamisa Kalombola alitoa kauli hiyo wakati wa kikao na watumishi wa NCAA, ambapo Tume hiyo ilikutana na watumishi kwa ajili ya kukumbushana kuhusu haki, wajibu, maadili na misingi ya utumishi wa umma.

Akiwa ameambatana na Katibu wa Tume ya Utumishi wa Umma, Bw. Nolasco Kipanda, pamoja na viongozi na watendaji wengine wa Tume hiyo, Jaji Mstaafu Kalombola alisisitiza kuwa utumishi wa umma ni dhamana inayohitaji kila mtumishi kutekeleza wajibu wake kwa uaminifu, weledi na kuzingatia maslahi mapana ya taifa.

“Kila mmoja ana wajibu wa kutekeleza kwa mwenzake ili kujenga utumishi wa umma wenye ufanisi na unaoaminika,” alisema Jaji Mstaafu Hamisa Kalombola.

Alisisitiza pia umuhimu wa watumishi kutunza siri za Serikali, kufanya kazi kwa uzalendo na kuzingatia uadilifu.

Kwa upande wake, Katibu wa Tume ya Utumishi wa Umma, Bw. Nolasco Kipanda, alisema Tume inaendelea kutekeleza jukumu lake la kufanya ukaguzi katika taasisi na mashirika ya umma kwa lengo la kuhakikisha sheria, kanuni, taratibu na misingi ya utumishi wa umma inazingatiwa.

Akizungumza katika kikao hicho naibu kamishna wa Uhifadhi wa NCAA Joas Makwati amesema mamlaka itafanyia kazi maelekezo ya Tume hiyo ili kihakikisha hakuna hoja za ukaguzi katika masuala ya utumishi na maeneo mengine.





























CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kimesema kitaendelea kuwa mfano wa demokrasia nchini, kikisisitiza kuwa misingi hiyo inaanza ndani ya Chama chenyewe.

CCM imesema imekuwa ikizingatia misingi ya demokrasia katika uendeshaji wa shughuli zake, ikiwemo katika mchakato wa uchaguzi wa viongozi wake.

Hayo yameelezwa na Makamu Mwenyekiti wa CCM - Bara, Stephen Wasira alipokuwa akifungua mafunzo ya Iitikadi na uenezi kwa makada wa Chama yaliyofanyika katika Chuo cha CCM, mkoani Iringa, jana.

Wasira akisema uchaguzi unaofanyika ndani ya CCM unalenga kutoa nafasi kwa wanachama kushiriki katika kuwachagua viongozi wanaowataka kwa mujibu wa taratibu zilizowekwa.

Alisema hatua hiyo ni sehemu ya kuhakikisha misingi ya demokrasia inaendelea kuimarika ndani ya Chama.

Aidha, alivitaka vyama vingine vya siasa nchini kuiga mfano huo kwa kuhakikisha vinazingatia demokrasia katika shughuli zake na uchaguzi wa viongozi wao.

Makamu Mwenyekiti Wasira alisisitiza kuwa, demokrasia ni muhimu katika kujenga vyama imara, vinavyoweza kuwajibika kwa wanachama na wananchi kwa ujumla.

Kwa upande mwingine, alisema CCM haiwezi kuingilia mihimili ya dola kwa kuwa kila mhimili una majukumu yake kwa mujibu wa Katiba na sheria.

Alieleza kuwa, Mahakama ni miongoni mwa mihimili inayopaswa kutekeleza majukumu yake kwa uhuru na kwa kuzingatia sheria.

Wasira alibainisha kwamba, kuheshimu mgawanyo wa madaraka ni sehemu muhimu ya uendeshaji wa nchi kwa misingi ya kikatiba.

Hivyo siyo sahihi kwa chama cha siasa kuingilia utekelezaji wa majukumu ya Mahakama au mhimili mwingine unaotambulika kikatiba.
















* Asisitiza GRID IMARA Simiyu ikamilike kwa wakati

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amewapongeza viongozi wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kwa kuhakikisha Kituo cha Kupokea, Kupooza na Kusambaza Umeme cha Imalilo pamoja na njia ya kusafirisha umeme kutoka Shinyanga hadi Simiyu vinaendelea kujengwa kwa kutumia wataalamu wa ndani.

"Hongereni sana TANESCO kwa uamuzi wenu wa kutekeleza ujenzi wa kituo hiki kwa kutumia wataalamu wa ndani baada ya changamoto zilizojitokeza katika utekelezaji wa mkataba na mkandarasi wa awali lakini pia niwapongeze na kazi mnayofanya. Ni nzuri. Ina standard na ubora," amesema.

Waziri Mkuu ametoa pongezi hizo leo (Jumanne, Septemba 15, 2026) baada ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa Kituo cha Imalilo na kupokea taarifa ya utekelezaji wa mradi huo, na kuongeza kuwa hatua hiyo imeonesha uwezo wa wataalamu wa Kitanzania katika kutekeleza miradi mikubwa kwa viwango vinavyostahili.

Waziri Mkuu ambaye yuko katika ziara ya kikazi mkoani Simiyu, ameiagiza TANESCO iongeze kasi ya utekelezaji wa Mradi wa Gridi Imara mkoani Simiyu na kuhakikisha Kituo cha Imalilo pamoja na njia ya kusafirisha umeme kutoka Shinyanga hadi Simiyu vinakamilika kwa wakati.

Amesema Serikali itahakikisha mtiririko wa fedha unaendelea ili kukamilisha njia hiyo ya kusafirisha umeme, akisisitiza kuwa kukamilika kwa kituo cha Imalilo bila kukamilika kwa njia ya kuleta umeme hakutatatua changamoto ya upatikanaji wa umeme mkoani Simiyu. "Fedha zipo, kazi ifanyike. Fanyeni kazi mchana na usiku ili kazi hii iishe kwa wakati," amesisitiza.

Waziri Mkuu amesema eneo linalohitaji msukumo mkubwa sasa ni kukamilika kwa njia ya kusafirisha umeme kutoka Ibadakuli, Shinyanga hadi Imalilo yenye urefu wa kilomita 110, ili kituo hicho kiweze kuanza kutoa huduma iliyokusudiwa. "Tutasukuma fedha kwenye njia ya kuleta umeme ili seti yote iweze kukamilika. Tukiweka tu transforma hapa bila kuwa na njia ya kuleta umeme tutakuwa bado hatujamaliza," amesema.

Amesema Simiyu ni mkoa wa kimkakati kwa uwekezaji katika viwanda kutokana na nafasi yake kijiografia na rasilimali zilizopo, hivyo kukamilika kwa mradi huo kutasaidia kuimarisha upatikanaji na ubora wa umeme pamoja na kuwezesha shughuli za kiuchumi. "Kilio cha kukatika katika umeme ni kikubwa sana. Na Simiyu ni mkoa wa kimkakati kwenye viwanda," amesema.

Waziri Mkuu amesema baada ya kurejea Dodoma atafanya kikao na Wizara ya Nishati na Wizara ya Fedha ili kuhakikisha mtiririko wa fedha haukwamishi utekelezaji wa mradi huo, huku akiwaagiza wakandarasi waongeze kasi ya kazi na kuhakikisha timu nzima inakuwa eneo la mradi wakati wote.

Akitoa taarifa ya utekelezaji wa mradi huo, Mkurugenzi Mtendaji Mkuu wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), Bw. Lazaro Twange amesema Kituo cha Imalilo kinajengwa kwa fedha za ndani kwa gharama ya sh. bilioni nane na hadi Septemba 13, 2026 utekelezaji wake umefikia asilimia 82.

Bw. Twange amesema TANESCO iliamua kutekeleza mradi wa kituo hicho chenye uwezo wa MVA 60, kV 220/33, kwa kutumia wataalamu wake wa ndani baada ya kutokukubaliana na masharti ya utekelezaji ya kampuni ya Xian Electric Engineering Company Limited iliyokuwa imepewa kazi hiyo awali.

Amesema njia ya kusafirisha umeme kutoka Ibadakuli, Shinyanga hadi Imalilo yenye urefu wa kilomita 110 na msongo wa kV 220 inagharimu sh. bilioni 48.7, huku utekelezaji wake ukiwa umefikia asilimia 60 na unatarajiwa kukamilika Februari, 2027.

Bw. Twange amesema mkandarasi ameshapeleka eneo la mradi takribani asilimia 90 ya vifaa vinavyohitajika na kazi za ujenzi wa misingi zimefikia zaidi ya asilimia 50, huku changamoto kubwa ikiwa ni upatikanaji wa fedha za kumlipa mkandarasi na wakandarasi wadogo.

Akizungumza kuhusu utekelezaji wa njia hiyo, mwakilishi mkazi wa kampuni ya Kalpataru Project International ya India, Bw. Ashish Tehran alisema ujenzi wa misingi umefikia asilimia 50 na ujenzi wa minara umeanza, huku vifaa vya mradi vikiwa vimewasili eneo la kazi.

Amesema pamoja na changamoto zilizopo katika baadhi ya misingi, wanaendelea na kazi na wanaamini watakamilisha mradi kwa wakati. Mradi huo pia unatarajiwa kutoa ajira kwa wananchi wa maeneo yanayotekelezwa, ikiwemo takribani ajira 200 kwa wakazi wa eneo la Bunamhala.





Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Ali Mwinyi, leo Septemba 15, 2026, ameungana na viongozi mbalimbali pamoja na wananchi katika Sala ya Jeneza ya Marehemu Bi. Maryam Shaaban Ramadhan, mama mzazi wa Katibu wa NEC, Idara ya Uchumi na Fedha ya CCM Taifa, Ndg. Jamal Kassim Ali.

Sala hiyo imefanyika katika Masjid Noor Muhammad, Kwa Mchina Mwanzo, Mkoa wa Mjini Magharibi, Zanzibar, ambapo Rais Dkt. Mwinyi amejumuika na ndugu, jamaa na wananchi kumuombea Marehemu kabla ya mazishi.

Aidha, Rais Dkt. Mwinyi ametoa pole kwa familia ya Marehemu, hususan Ndg. Jamal Kassim Ali, ndugu, jamaa na wote walioguswa na msiba huo, huku akiwataka kuwa na subira na ustahimilivu katika kipindi hiki kigumu cha majonzi.













Top News