WAZIRI wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda, ameitaka Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU) kuimarisha mfumo wa udahili na usajili wa wanafunzi wa elimu ya juu ili kuhakikisha vyuo havipokei wanafunzi zaidi ya uwezo wa miundombinu na wakufunzi waliopo.
Prof. Mkenda amesema hatua hiyo ni muhimu katika kulinda ubora wa elimu ya juu nchini, huku ikihakikisha wanafunzi wanapata nafasi za masomo kwa haki, uwazi na kwa kuzingatia uwezo halisi wa kila chuo.
Waziri huyo ameyasema hayo leo, Septemba 5, 2026, jijini Dodoma, baada ya kukutana na Makamu Wakuu wa Vyuo Vikuu pamoja na Wenyeviti wa Mabaraza ya vyuo vikuu nchini katika kikao kilichojadili masuala mbalimbali yanayohusu sekta ya elimu ya juu, ikiwemo udahili na usajili wa wanafunzi.
Amesema Serikali inalenga kuhakikisha mfumo wa udahili unakuwa bora na wenye ufanisi, ili kuepusha changamoto zinazoweza kujitokeza pale vyuo vinapodahili wanafunzi wengi kuliko uwezo wa kuwahudumia.
“Tumefanya hivyo kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunatengeneza mfumo mzuri ambao hautaleta utata, hautakuwa na kuweka idadi ya wanafunzi kuliko uwezo wa kufundisha,” amesema Prof. Mkenda.
Prof. Mkenda amewataka wanafunzi wanaotarajia kujiunga na vyuo vikuu kuendelea kufanya maombi yao wakati wakisubiri maelekezo zaidi kutoka TCU kuhusu utaratibu wa udahili.
Amesema mfumo unaoandaliwa unalenga kuweka uwiano kati ya ongezeko la mahitaji ya elimu ya juu na uwezo wa vyuo kutoa elimu bora, huku maslahi ya wanafunzi yakilindwa.
Serikali kuongeza nafasi za elimu ya juu
Waziri Mkenda amesema Serikali inaendelea kuongeza uwezo wa vyuo vikuu nchini kupitia ujenzi na upanuzi wa kampasi katika mikoa mbalimbali ili kuongeza nafasi za wanafunzi kupata elimu ya juu.
Amesema uwekezaji huo utawezesha vijana wengi zaidi kupata fursa za masomo bila kulazimisha vyuo kupokea idadi kubwa ya wanafunzi ambayo inaweza kuathiri ubora wa elimu.
Kwa mujibu wa Prof. Mkenda, Tanzania bado haijafikia kiwango cha uandikishaji wa wanafunzi katika elimu ya juu kinacholengwa, hivyo Serikali itaendelea kuongeza nafasi za masomo sambamba na kuhakikisha viwango vya elimu vinadumishwa.
Amesema lengo ni kujenga mfumo wa elimu ya juu unaotoa fursa kwa vijana wengi zaidi na wakati huo huo kuwaandaa kwa ufanisi ili waweze kukidhi mahitaji ya soko la ajira
TCU YAWEKA MKAZO KWENYE UDAHILI WA 2026/2027
Kwa upande wake, Katibu Mtendaji wa TCU, Prof. Charles Kihampa, amesema kikao hicho kimejadili kwa kina masuala ya udahili wa wanafunzi, ubora wa elimu pamoja na hatua mbalimbali zinazochukuliwa na Serikali katika kuendeleza sekta ya elimu ya juu.
Amesema TCU, Serikali na vyuo vikuu wamekubaliana kuendelea kushirikiana katika kuboresha mifumo ya udahili kwa kuzingatia mabadiliko na mahitaji yanayoendelea katika sekta ya elimu.
Prof. Kihampa amesema ongezeko linalotarajiwa la wanafunzi kutokana na mabadiliko mbalimbali ya sera linahitaji maandalizi ya mapema kutoka kwa Serikali, TCU na vyuo vikuu ili kuhakikisha uwezo wa kutoa elimu unaendana na idadi ya wanafunzi wanaotarajiwa.
Naye Mwenyekiti wa Baraza la Chuo Kikuu cha Teolojia cha Lweru, Aggrey Mlimuka, amesisitiza umuhimu wa vyuo vikuu kusimamia ubora wa elimu na kuhakikisha wahitimu wanakuwa na maarifa, uwezo na weledi unaokidhi mahitaji ya soko la ajira.
Amesema kila chuo kina wajibu wa kuhakikisha programu zake zinazalisha wataalamu wenye uwezo, akibainisha kuwa endapo ubora hautasimamiwa, soko la ajira litawachuja wahitimu kwa kuzingatia uwezo wao.
DIRISHA LA PILI LA UDAHIL KUFUNGULIWA WIKI IJAYO
Awali, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Ushirika Moshi (MoCU), Prof. Alfred Sife, amesema vyuo vikuu vimekubaliana kuendelea kuboresha mchakato wa udahili kwa mwaka wa masomo 2026/2027 ili kuhakikisha wanafunzi wanaodahiliwa wanakidhi vigezo na wanajiunga na programu zinazolingana na sifa zao.
Prof. Sife amesema moja ya hoja kubwa iliyojadiliwa katika kikao hicho ni mwenendo wa udahili unaoendelea, ambapo dirisha la kwanza la maombi limekamilika na dirisha la pili linatarajiwa kufunguliwa wiki ijayo.
Amesema kuimarishwa kwa mfumo huo kutasaidia kuhakikisha wanafunzi wenye sifa wanapata nafasi katika programu na vyuo vinavyowafaa, huku taratibu, kanuni na sheria za udahili zikizingatiwa.
Ameongeza kuwa ushirikiano kati ya Serikali, TCU na vyuo vikuu ni muhimu katika kuboresha mifumo ya elimu na kuhakikisha uwekezaji unaofanywa katika sekta hiyo unazalisha wahitimu wenye uwezo wa kukidhi mahitaji ya taifa na soko la ajira.









.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)



.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)








.jpeg)



.jpeg)


.jpeg)



.jpeg)


