Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Hamad Chande, ameipongeza Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) kwa mchango wake katika kuwawezesha wakulima kupata masoko yenye ushindani kupitia Mfumo wa Stakabadhi za Ghala.

Mhe. Chande ameyasema hayo leo Agosti 6, 2026, baada ya kutembelea banda la WRRB katika Maonesho ya 88 yanayoendelea katika Viwanja vya Dkt. John Malecela, jijini Dodoma.

Amesema WRRB imeendelea kuwa nyenzo muhimu katika kuimarisha biashara ya mazao kwa kuwawezesha wakulima kupata masoko yenye ushindani, kuongeza thamani ya mazao yao na kuchangia ukuaji wa uchumi wa taifa.

Aidha, ameipongeza WRRB kwa kuendelea kutoa elimu kwa wananchi na kutoa wito kwa wadau wa sekta ya kilimo kuendelea kutekeleza kwa vitendo kauli mbiu ya Maonesho ya Nane Nane ya mwaka 2026 isemayo, "Tambua Soko, Ongeza Tija, Tekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050," kwa kuimarisha mifumo ya masoko, kuongeza tija katika uzalishaji na kuhakikisha wakulima wananufaika na fursa zilizopo katika mnyororo wa thamani wa mazao.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Uratibu Huduma ,Bw. Mwita Thomas ameeleza kuwa WRRB itaendelea kuboresha huduma zake, kuimarisha usimamizi wa mfumo huo kwa kushirikiana na wadau ili kuhakikisha sekta ya kilimo inakuwa chachu ya maendeleo ya uchumi na ustawi wa wananchi.

DODOMA

Mfumo wa kuagiza mafuta kwa ajili ya matumizi ya miezi miwili inayofuata umeiwezesha Tanzania kuendelea kuwa na bidhaa za mafuta za kutosha, licha ya vita na changamoto nyingine zinazoathiri soko la dunia.

Hayo yameelezwa na Mhandisi Rehema Mahundi katika siku ya sita ya Maonesho ya Nanenane yanayoendelea jijini Dodoma, wakati akitoa elimu kwa wananchi waliotembelea Banda la Wakala wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (PBPA).

Mhandisi Mahundi alisema moja ya maswali yanayoulizwa zaidi na wananchi ni namna Mfumo wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja unavyoiwezesha nchi kuwa na uhakika wa upatikanaji wa mafuta, hasa wakati wa migogoro na vita katika maeneo mbalimbali duniani.

Akijibu swali hilo, alieleza kuwa PBPA hutangaza zabuni kila mwezi kwa ajili ya kuagiza mafuta yatakayotumika nchini katika miezi miwili inayofuata. Utaratibu huo unajulikana kama M+2.

“PBPA huingia mikataba na wazabuni walioshinda zabuni hizo ili kuhakikisha bidhaa za mafuta zinafika nchini kwa wakati, hata changamoto zinapojitokeza katika soko la dunia,” alisema Mhandisi Mahundi.

Alisema kupitia mfumo huo, Tanzania imeendelea kuwa na uhakika wa upatikanaji wa mafuta wakati wote na kwa gharama zinazoakisi hali halisi ya soko la dunia.

Katika Maonesho ya Nanenane, PBPA imeendelea kutoa elimu kuhusu Mfumo wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja kwa watu kutoka makundi mbalimbali, wakiwamo wanafunzi, wakulima, wajasiriamali, wafanyabiashara pamoja na wawakilishi kutoka taasisi za elimu na sekta binafsi.

Mhandisi Mahundi amewakaribisha wananchi kutembelea Banda la PBPA katika Viwanja vya Nanenane jijini Dodoma ili kupata elimu zaidi kuhusu namna mfumo huo unavyosimamia mnyororo wa uagizaji, usimamizi na upokeaji wa bidhaa za mafuta nchini.
Na Avila Kakingo
SERIKALI imesema Jukwaa la Miundombinu Afrika (Infra for Africa Forum) limekamilika kwa mafanikio makubwa, huku sasa ikielekeza nguvu kwenye Mkutano Mkuu wa Wanahisa wa Taasisi ya Africa50 unaofanyika leo Agosti 6, 2026.

Akizungumza jijini Dar es Salaam, Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omar, amesema baada ya kukamilika kwa jukwaa hilo la siku mbili lililofunguliwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, wanahisa wa Africa50 wanakutana kujadili masuala ya uongozi na mwelekeo wa taasisi hiyo. Alisema yeye atakuwa mwenyekiti mwenza wa mkutano huo pamoja na Rais wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), Dkt. Sidy Ould Tah.

Waziri huyo amesema jukwaa hilo limewakutanisha viongozi wa serikali, taasisi za fedha za maendeleo, wawekezaji wa sekta binafsi na wadau wa kimataifa kujadili namna ya kuziba pengo la miundombinu barani Afrika na kuimarisha ushirikiano katika kugharamia miradi ya maendeleo. Aliongeza kuwa mjadala wa mwisho ulijikita katika mustakabali wa ushirikiano wa kimataifa (multilateralism), ambapo ilisisitizwa kuwa Afrika inapaswa kuongeza uwezo wa kujitegemea katika kufadhili na kutekeleza miradi yake ya maendeleo.

Aidha, amesema Tanzania imenufaika na mkutano huo kwa kusaini makubaliano matatu muhimu. Makubaliano hayo yanahusu ushirikiano kati ya TANESCO na Africa50 katika miradi ya usafirishaji wa umeme (transmission), mradi wa Mini LNG kati ya TPDC, Taqa Arabia na Africa50 kwa ajili ya kuchakata gesi asilia na kuiwezesha kutumika zaidi katika viwanda vya ndani, pamoja na makubaliano ya ujenzi wa kituo kipya cha huduma za usafishaji wa figo (dialysis) ili kukabiliana na ongezeko la magonjwa yasiyoambukiza nchini.

Balozi Khamis amesema kukamilika kwa jukwaa hilo na kutiwa saini kwa makubaliano hayo kunaonesha dhamira ya Tanzania ya kuendelea kushirikiana na wadau wa maendeleo katika kuimarisha miundombinu, sekta ya nishati na huduma za afya kwa manufaa ya wananchi na ukuaji wa uchumi.






Na Mwandishi Wetu

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk.Samia Suluhu Hassan na Yoweri  Museveni wa Uganda wameshuhudia utiaji saini wa Hati ya Makubaliano (MoU) ya kuendeleza ujenzi wa kiwanda cha kusafisha mafuta na Kitovu cha Nishati cha Kikanda Jijini  Tanga, mradi unaotarajiwa kubadili taswira ya sekta ya nishati Afrika Mashariki.

Makubaliano hayo yaliyosainiwa na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), Kampuni ya Taifa ya Mafuta ya Uganda (UNOC) na kampuni ya VTTO Bahrain, yanafungua njia kwa hatua za awali za kitaalamu na uwekezaji katika ujenzi wa miundombinu hiyo muhimu.

Akizungumza katika hafla hiyo,leo Ikulu jijini Dar es Salaam Waziri wa Nishati Deogratias Ndejembi alisema makubaliano hayo ni hatua muhimu katika kuimarisha ushirikiano wa Tanzania na Uganda kwenye sekta ya nishati.

Njejembi amesema kuwa mradi huo  unatarajiwa kujumuisha kiwanda cha kusafisha mafuta, miundombinu ya kuhifadhi bidhaa za petroli, huduma za usafirishaji pamoja na bomba la kusafirisha bidhaa za mafuta linaloweza kufanya kazi kwa pande zote mbili kati ya Tanzania na Uganda.

Amesema kuwa utekelezaji wa mradi huo unalenga kuifanya Tanga kuwa kituo muhimu cha usambazaji wa bidhaa za mafuta kwa nchi za Afrika Mashariki na ukanda mpana wa Afrika.

"Utiaji saini wa leo siyo tu makubaliano, bali ni msingi mwingine wa mageuzi ya kiuchumi katika Afrika Mashariki," alisema.

Alisema mradi huo unaendeleza ushirikiano ulioanza kupitia Mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP), wenye thamani ya takribani dola za Marekani bilioni sita, unaolenga kusafirisha mafuta ghafi kutoka maeneo ya uzalishaji nchini Uganda hadi Bandari ya Tanga.

Ndejembi alisema tofauti na EACOP ambayo inalenga kusafirisha mafuta ghafi, Kitovu cha Nishati cha Tanga kitasaidia kuongeza thamani ya rasilimali hiyo kupitia usafishaji wa mafuta, uhifadhi, usafirishaji na biashara ya bidhaa za petroli.

"Mradi huu ukikamilika una uwezo wa kuvutia uwekezaji unaozidi dola za Marekani bilioni 20, kuunda ajira, kuchochea ukuaji wa viwanda na kuimarisha usalama wa nishati katika ukanda huu," alisema.

Ndejembi aliongeza mradi huo unaendana na maono ya Rais Samia ya kuifanya Tanga kuwa kitovu cha biashara ya mafuta Afrika Mashariki kutokana na nafasi yake ya kimkakati, ikiwemo kuwa lango la Bahari ya Hindi na eneo la kupokea bomba la EACOP.

Kwa upande wake, Waziri wa Nishati na Maendeleo ya Madini wa Uganda, Dk Ruth Nankabirwa Ssentamu, alisema makubaliano hayo yanaonyesha dhamira ya nchi hizo mbili ya kushirikiana katika kuongeza thamani ya rasilimali na kukuza uchumi wa kikanda.

"Hatupaswi kuuza malighafi pekee. Tunapaswa kujenga viwanda, kuunda ajira zenye ujuzi na kuhakikisha wananchi wetu wanapata manufaa makubwa kutokana na rasilimali hizi," alisema.

Dk Nankabirwa alisema kiwanda cha kusafisha mafuta kinachopangwa kujengwa Kabaale nchini Uganda na Kitovu cha Nishati cha Tanga havitashindana, bali vitakamilishana kwa kuongeza uwezo wa usafishaji wa mafuta na kuimarisha upatikanaji wa nishati katika Afrika Mashariki.

Aliongeza kuwa Tanzania na Uganda zinaendelea na utekelezaji wa miradi mingine ya pamoja, ikiwemo bomba la kusafirisha bidhaa za mafuta, bomba la gesi asilia kati ya nchi hizo mbili na mradi wa njia ya kusafirisha umeme wa kilovolti 400.

Utiaji saini wa makubaliano hayo ni hatua nyingine katika ushirikiano wa muda mrefu wa Tanzania na Uganda kwenye sekta ya nishati ulioimarishwa kupitia EACOP mwaka 2017.








Na Avila Kakingo
RAIS Mstaafu wa Awamu ya Nne, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, amesema Afrika inaweza kukosa kunufaika na ajira milioni 250 zinazotarajiwa kuzalishwa na uchumi wa kidijitali duniani iwapo haitawekeza katika kuwajengea vijana ujuzi wa teknolojia za kisasa, hususan Akili Mnemba (Artificial Intelligence–AI).

Akizungumza katika Jukwaa la Miundombinu Afrika lililofanyika sambamba na Mkutano Mkuu wa Wanahisa wa Africa50 jijini Dar es Salaam, leo Agosti 06, 2026 Dkt. Kikwete amesema mustakabali wa ajira duniani unategemea zaidi uwezo wa watu kumiliki ujuzi wa kidijitali.

"Kutakuwa na ajira milioni 250 za kidijitali, lakini zitapatikana kwa watu wenye ujuzi. Tusipowekeza katika elimu na kuwajengea vijana wetu uwezo huo, hatutaweza kuzipata fursa hizo."

Pia amesema dunia imehama kutoka kwenye mjadala wa upatikanaji wa intaneti na sasa inaingia katika enzi ya Akili Mnemba, teknolojia ambayo inaendelea kubadili namna ya uzalishaji, utoaji wa huduma na ukuaji wa uchumi.

"Leo hii habari kubwa duniani ni Artificial Intelligence. Hatuwezi kubaki kwenye matumizi ya kawaida ya intaneti wakati dunia imekwenda hatua nyingine. Lazima nasi tujiandae kuitumia teknolojia hiyo kusukuma maendeleo yetu," amesema.

Dkt. Kikwete amesema AI inaweza kuwa chachu ya maendeleo katika sekta mbalimbali zikiwemo kilimo, afya, uhandisi, elimu na maeneo mengine ya uzalishaji, endapo mataifa ya Afrika yatawekeza katika elimu, utafiti na ubunifu.

Aidha, amesisitiza kuwa mageuzi ya kidijitali yanapaswa kuwa sehemu ya mipango ya maendeleo ya miundombinu ya Afrika, akieleza kuwa bara hilo linapaswa kujiandaa kwa uchumi unaotegemea maarifa na teknolojia.

Vilevile, amekumbusha kuwa viongozi wa Afrika walikubaliana kupitia Dira ya Afrika 2063 kujenga bara lenye maendeleo jumuishi na miundombinu ya kisasa, huku taasisi ya Africa50 ikiwa miongoni mwa vyombo vinavyoongoza juhudi za kuharakisha uwekezaji katika miradi ya kimkakati ya miundombinu.

Dkt. Kikwete amesema Tanzania imepata heshima ya kuwa mwenyeji wa mkutano huo muhimu unaowakutanisha viongozi wa serikali, wawekezaji na wadau wa maendeleo kujadili namna ya kuharakisha maendeleo ya miundombinu na uchumi wa bara la Afrika.



Na Mwandishi Wetu

TANZANIA imeidhinisha  miradi minne ya biashara ya kaboni yenye thamani ya zaidi ya Shilingi bilioni 135.5, ikifungua njia ya mauzo  ya kaboni katika soko la kimataifa.

Miradi hiyo imeidhinishwa chini ya Kifungu cha 6 cha Mkataba wa Paris kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi, kinachoruhusu nchi kushiriki biashara ya kimataifa ya mikopo ya kaboni kama sehemu ya juhudi za kupunguza uzalishaji wa gesi chafuzi.

Akizungumza jijini Dar es Salaam, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Hamad Yussuf Masauni, alisema idhini hiyo ilitolewa baada ya Kamati ya Kitaifa ya Tathmini ya Miradi ya Kaboni kukamilisha uchambuzi wa kitaalamu na kupendekeza miradi hiyo kwa Serikali.

Kwa mujibu wa Masauni, Serikali itanufaika na zaidi ya dola milioni 4.2 (Shilingi bilioni 10.8) kupitia mgao wake wa asilimia nane wa mapato yatokanayo na mauzo ya mikopo ya kaboni, kama inavyoelekezwa na Kanuni za Biashara ya Kaboni za mwaka 2022.

Miradi hiyo inatekelezwa na Burn Manufacturing Company Ltd, UpEnergy Group kwa kushirikiana na Sayari Safi Ltd, Water Mission International Tanzania pamoja na Bridge Carbon TZ Co. Limited.

 Miradi hiyo inalenga kuongeza matumizi ya nishati safi ya kupikia na kupanua upatikanaji wa maji salama, huku ikipunguza uzalishaji wa hewa ukaa.

Zaidi ya majiko banifu 900,000, yakiwemo ya umeme, yatasambazwa kwa zaidi ya kaya 600,000 katika maeneo ya mijini na vijijini. 

Hatua hiyo inatarajiwa kuongeza matumizi ya nishati safi ya kupikia na kusaidia utekelezaji wa mkakati wa Serikali wa kuhakikisha asilimia 80 ya Watanzania wanatumia nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034.

Sambamba na hilo, mradi wa maji safi utakaotekelezwa katika mikoa yote 26 unatarajiwa kuwafikia zaidi ya kaya milioni moja, kuunda ajira za moja kwa moja 1,000, kushirikisha zaidi ya wasambazaji 100 na kuzalisha ajira nyingine 350 wakati wa utekelezaji.

Kwa mujibu wa tathmini ya Serikali, miradi hiyo kwa pamoja itapunguza kati ya tani milioni moja na mbili za hewa ukaa sawa (tCO₂e) kila mwaka, hatua itakayochangia utekelezaji wa Malengo ya Kitaifa ya Kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi pamoja na ahadi za Tanzania chini ya Mkataba wa Paris.

Masauni alisema Tanzania imeendelea kuimarisha mfumo wa usimamizi wa biashara ya kaboni kwa kuanzisha Kituo cha Taifa cha Ufuatiliaji wa Kaboni, huku miradi 117 ikiwa tayari imesajiliwa hadi Julai 2026.

 Alisema ongezeko hilo linaashiria kuimarika kwa mazingira ya uwekezaji na kuongezeka kwa imani ya wawekezaji katika sekta hiyo.

Aliongeza kuwa Serikali inaendelea kupitia maombi mengine ya miradi katika sekta za misitu, kilimo kinachostahimili mabadiliko ya tabianchi, urejeshaji wa ardhi, usimamizi wa taka, biochar, usafiri na miundombinu ya magari ya umeme ili kupanua wigo wa biashara ya kaboni nchini.

Aliwataka wawekezaji wa ndani na nje ya nchi kutumia fursa zinazotokana na mfumo wa udhibiti ulioimarishwa na ushiriki wa Tanzania katika Kifungu cha 6 cha Mkataba wa Paris, akisema hatua hizo zinaifanya Tanzania kujijengea nafasi kama moja ya vituo muhimu vya uwekezaji wa biashara ya kaboni barani Afrika.



Na Janeth Raphael - MichuziTv 

Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu),  Ummy Nderiananga, amewataka wananchi kutumia Maonesho ya Kimataifa ya Wakulima Nanenane 2026 kama fursa ya kujifunza huduma na mipango mbalimbali ya Serikali inayolenga kuboresha maisha yao.

Nderiananga ametoa wito huo alipotembelea Banda Jumuishi la Ofisi ya Waziri Mkuu pamoja na taasisi zake katika Viwanja vya Dkt. John Samuel Malecela, jijini Dodoma, Agosti 6, 2026.

Akiwa katika banda hilo, aliwapongeza waandaaji kwa maandalizi mazuri na namna wanavyotoa huduma kwa wananchi kupitia elimu, ushauri na mwongozo unaowawezesha kupata suluhisho la changamoto mbalimbali pamoja na kuunganishwa na taasisi husika kwa haraka.

Amesema ushiriki wa taasisi zote zilizo chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu katika maonesho hayo unaonyesha dhamira ya Serikali ya kusogeza huduma karibu na wananchi, huku akiwakaribisha wakazi wa Dodoma na maeneo mengine nchini kutembelea banda hilo ili kujionea kazi zinazotekelezwa chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Nderiananga pia aliwahamasisha wananchi kutembelea maonesho hayo kwa wingi ili kupata uelewa mpana kuhusu majukumu ya Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zake, sambamba na kujifunza fursa zinazopatikana katika sekta za kilimo na mifugo ambazo ni nguzo muhimu za maendeleo ya uchumi.

Maonesho ya Kimataifa ya Wakulima Nanenane 2026 yanaendelea katika viwanja vya Dkt. John Samuel Malecela, jijini Dodoma, yakiongozwa na kaulimbiu isemayo, "Tambua Soko, Ongeza Tija Kutekeleza Dira 2050."










Mkurugenzi wa Uthibiti Ubora wa Shule, Dkt. Ephraim Simbeye,akizungumza wakati akifungua kikao kazi cha Wakuu wa Vyuo vya Ualimu vya Serikali na visivyo vya Serikali pamoja na Waratibu wa Taaluma jijini Dodoma, leo Agosti 6, 2026, kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia,

Na.Mwandishi wetu-

Serikali imesisitiza kuwa ubora wa walimu wanaoandaliwa katika vyuo vya ualimu ndio utakaoamua mustakabali wa elimu nchini katika miaka ijayo.

Akifungua kikaokazi cha Wakuu wa Vyuo vya Ualimu vya Serikali na visivyo vya Serikali pamoja na Waratibu wa Taaluma jijini Dodoma, Agosti 6, 2026, kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mkurugenzi wa Uthibiti Ubora wa Shule, Dkt. Ephraim Simbeye, amewataka Wakuu wa vyuo kuimarisha usimamizi wa mafunzo ili kuhakikisha wahitimu wanakuwa na umahiri, maadili na stadi zinazokidhi mahitaji ya Taifa.

Ameongeza kuwa vyuo vya Ualimu vina jukumu kubwa katika utekelezaji wa mtaala kwa kuhakikisha walimu wanaohitimu wanakidhi viwango hitajika.

Dkt. Simbeye ameeleza kuwa kikaokazi hicho kimefanyika katika kipindi muafaka baada ya kukamilika kwa mzunguko wa kwanza wa wahitimu wa Mtaala Ulioboreshwa wa Elimu ya Ualimu ulioanza kutekelezwa mwaka 2023 na kusema kuwa hatua hiyo inatoa nafasi ya kutathmini mafanikio, changamoto na maeneo yanayohitaji maboresho.

Kiongozi huyo amesema kuwa Wakuu wa Vyuo wanapaswa kuwa wabunifu katika matumizi ya rasilimali. Ushirikiano na sekta binafsi pamoja na kuanzisha miradi ya uzalishaji mali bila kuathiri utoaji wa elimu.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa kuzingatia miongozo ya Serikali katika utekelezaji wa mtaala, mafunzo kwa vitendo na utoaji wa mafunzo kwa njia ya masafa, ili kuhakikisha nchi inapata walimu wenye viwango vinavyofanana vya umahiri, maadili na uzalendo.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Elimu ya Ualimu na Mafunzo, Mathias Mvula, amesema lengo la kikao kazi hicho ni kubadilishana uzoefu uliopatikana katika utekelezaji wa mtaala ulioboreshwa wa Elimu ya Ualimu.


Top News