Dodoma
JARIBIO la kwanza la Mbegu ya viazi mviringo lililotafitiwa na Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI) limeonesha mafanikio makubwa mkoani Dodoma katika shamba la Makamu wa Rais Mstaafu Mhe. Dkt Philip Mpango lililopo Kijiji cha Mayamaya, Wilaya ya Bahi mkoani Dodoma.

Jaribio hilo lililochukua siku 104 za majaribio shambani hadi kuvuna limedhihirisha kuwa zao la viazi mviringo linaweza kustawi katika mazingira ya Mkoa wa Dodoma na kuufanya Mkoa huo kuwa na fursa mpya ya zao la chakula na biashara ambalo linaweza kuwasaidia wananchi wa mkoa huo kuondokana na umasikini.

Akiongelea kuhusu jaribio hilo na matokeo yake, Makamu wa Rais Mstaafu Mhe. Dkt. Philip Mpango, ameishukuru TARI kwa kusimamia jaribio hilo ambalo kwa mara ya kwanza limeonyesha mafanikio katika Kijiji cha Mayamaya na kuwataka wakazi wa Mkoa wa Dodoma kuchangamkia fursa ya kulima zao hilo pindi utafiti utakapokamilika.

“ Wakazi wa Dodoma sasa tuanze kuchangamkia hii fursa na TARI wako tayari kutusaidia kwa kutupatia mbegu bora zinazofaa zaidi na hii itatusaidia chakula na kipato kwa ajili ya kusaidia watoto wetu kwenda shule. Dodoma sio nusu jangwa, ni maarifa tu ya kupata na kuvuna maji kwa ajili ya kuendeleza kilimo chetu, hatuwezi kuendelea kwa kutegemea mtama, mahindi, zabibu au alizeti pekee lazima tuongeze na mazao mengine” alisema Mhe. Dkt. Mpango.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa TARI, Dkt. Thomas Bwana amemshukuru Mhe. Dkt. Mpango kwa kukubali TARI kuweka jaribio la viazi mviringo katika shamba lake lililopo katika Kijiji cha Mayamaya na kueleza kuwa kwa sasa TARI imepanga kuweka majaribio ya zao hilo kwa wakulima wadogo wanaolima kwa kutegemea mvua.

Katika hatua nyingine Dkt. Bwane ameongeza kuwa TARI itaendelea na majaribio ya utafiti wa mazao katika maeneo mbalimbali nchini ili kuondoa dhana iliyojengeka ya ikolojia hii ni ya mazao Fulani pekee na kuwaomba wananchi hususan wakulima kuwakaribisha TARI kuweka majaribio ya utafiti katika mashamba yao.

Kwa mujibu wa Mtafiti Kiongozi wa zao la viazi mviringo kutoka kituo cha TARI - Uyole Dkt. Owekisha Kwigizila, mbegu hiyo mpya ya TARI ina sifa ya kukomaa kwa muda mfupi wa takribani siku 90, kustahimili ukame na baadhi ya magonjwa pamoja na kuwa na uwezo wa kuzalisha tani 35 hadi 40 kwa hekta moja.

Baadhi ya wakazi wa Kijiji cha Mayamaya walioshiriki katika zoezi la uvunaji wa viazi hivyo wameonesha kustaajabishwa na kustawi kwa zao hilo katika Kijiji hicho cha Mayamaya na kueleza kuwa hiyo ni mara yao ya kwanza kuona zao hilo la viazi likilimwa na kustawi Mkoani Dodoma na kuonyesha shauku kubwa ya kujaribu kulima zao hilo katika mashamba yao,

Utafiti huo wa zao la viazi Mkoani Dodoma bado unaendelea ili kukamilisha hatua zote muhimu kabla ya mbegu hiyo kuingizwa rasmi sokoni. Mafanikio hayo yanaendelea kuthibitisha kuwa Dodoma inaweza kuzalisha mazao mbalimbali ya chakula na biashara kupitia nguvu ya utafiti, ubunifu na teknolojia za kilimo na kubadilisha maisha ya wakulima wa Mkoa wa Dodoma.

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
JUMUIYA ya Khoja Shia Ithna-Asheri Mkoa wa Dar es Salaam imeandaa Kambi ya Afya na Macho pamoja na Mafunzo ya Imam Hussein (a.s), yatakayofanyika kwa Agasti 14 hadi Agasti 16 katika Viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam.

Kambi hiyo inayotolewa bure inalenga kuwafikishia wananchi huduma muhimu za afya, hususan wale ambao hawana uwezo wa kuzipata kwa urahisi.

Akizungumza kuhusu kambi hiyo, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Khoja Shia Ithna-Asheri Mkoa wa Dar es Salaam, Alhaj Mohamedraza Dewji, amesema shughuli hiyo ni sehemu ya jitihada za jumuiya hiyo za kutoa huduma kwa jamii bila kujali dini, kabila wala hali ya maisha.

Amesema kambi hiyo, ambayo mwaka jana ilihudumia maelfu ya wananchi, itawakutanisha wataalamu wa afya, taasisi mbalimbali pamoja na mashirika ya tiba kutoka ndani ya Tanzania kwa lengo la kuwafikia wananchi wengi zaidi.

“Huduma hizi zitatolewa bila gharama yoyote na zinalenga kuwahudumia wananchi wote bila kujali dini, kabila au hali ya maisha,” amesema Mohamedraza.

Amesema katika kambi hiyo wananchi watapata huduma mbalimbali, zikiwemo uchunguzi wa macho, vipimo vya sukari, shinikizo la damu, uzito na urefu (BMI) pamoja na uchunguzi wa ugonjwa wa mtoto wa jicho (cataract).

Aidha, amesema wananchi wenye uhitaji watapatiwa miwani na dawa bure, huku wanawake wakipata huduma za uchunguzi wa saratani ya matiti na shingo ya kizazi kwa kushirikiana na Taasisi ya Saratani Ocean Road.

Kwa mujibu wa Mwenyekiti huyo, pia kutakuwa na elimu kuhusu afya ya akili pamoja na zoezi la uchangiaji damu litakalofanyika kwa kushirikiana na Taasisi ya Damu Salama.

KUMBUKUMBU YA IMAM HUSSEIN
Mohamedraza amesema jina la kambi hiyo limechukuliwa kutoka katika historia ya Imam Hussein (a.s), mjukuu wa Mtume Muhammad (s.a.w), ambaye alifariki katika tukio la Karbala lililotokea mwaka 61 Hijria (A.H).

Amesema tukio la Karbala limeendelea kuwa kumbukumbu muhimu kwa wafuasi wa Ahlulbayt na watu wengine, likisisitiza misingi ya haki, huruma, utu na kujitolea kwa ajili ya wengine.

“Lengo ni kugeuza mafunzo ya Karbala kuwa vitendo vya huruma vinavyogusa maisha ya watu, hasa walioko pembezoni,” amesema.

Amesema utoaji wa huduma za afya bila malipo ni miongoni mwa njia zinazotumiwa na jumuiya hiyo kuhuisha mafunzo na urithi wa Imam Hussein (a.s) kwa vitendo vinavyomnufaisha mwanadamu.

Kwa mujibu wa baadhi ya washiriki wa kambi hiyo katika miaka iliyopita, shughuli hiyo imekuwa zaidi ya utoaji wa huduma za afya, kwa kuwa imekuwa pia sehemu ya kuwakutanisha watu kutoka makundi mbalimbali kwa msingi wa utu, huruma na kusaidiana.

Jumuiya ya Khoja Shia Ithna-Asheri Jamaat Mkoa wa Dar es Salaam, ikiwa miongoni mwa jamii za Waislamu wa Shia na wafuasi wa Ahlulbayt, imekuwa ikifanya shughuli mbalimbali za kijamii kwa kusaidia wagonjwa, wahitaji na makundi yenye uhitaji.

Kwa mujibu wa jumuiya hiyo, kambi hiyo ni sehemu ya kuendeleza dhamira ya kusaidia jamii kupitia matendo ya huruma na huduma za kibinadamu, huku ikisisitiza kuwa huduma hizo zinapaswa kupatikana kwa heshima na bila ubaguzi.

 


Shirika la Madini la Taifa ( STAMICO) katika muendelezo  wa kuhakikisha linaendelea kuwa kinara  katika kuhamasisha matumizi ya Nishati Safi Tanzania nzima, leo tarehe 11/8/2026  imeingia mkataba mnono  wa pande tatu kati ya  STAMICO, Chuo cha Mafunzo  na taasisi ya FDH  ya kuhakikisha magereza yote ya Zanzibar  yanaanza kutumia Nishati ya Rafiki  Briquettes.

Makubaliano hayo yamefanyika katika ukumbi wa Chuo cha Mafunzo Zanzibar  na kushuhudiwa  na Kamishna  wa Magereza  Zanzibar Khamis Abdalah Khamis pamoja na  Mkurugenzi  Mtendaji  wa STAMICO  Dkt Venance  Mwasse na  Mkurugenzi  wa FDH  Bwn Michael Salali.

Akiongea katika hafla hiyo, Dkt Mwasse ameipongeza  taasisi ya FDH kwa kufanikisha kuingia makubaliano  haya ambayo yatawezesha Magereza  zote za Zanzibar  kupata Nishati hii ya Rafiki Briquettes  ambayo  inaenda kuleta afueni kwenye  gharama za Nishati kwa Magereza   lakini pia kuanza kutekeleza agenda ya Nishati Safi kwa taasisi zote zinazohudumia watu zaidi ya 100.

"Suala la Nishati Safi ni  Agenda ya Kitaifa na sisi STAMICO  tumeibeba kwa mikono miwili kuhakikisha tunatumia Nishati yetu ya Rafiki Briquettes  kuhamasisha matumizi ya Nishati Safi" amesema Dkt Mwasse 

Dkt Mwasse  pia ameahidi kusaidia kuleta mafunzo na Kongamano  la  kuhamasisha  matumizi  ya Nishati Nzima kwa Watumishi wa Magereza na Wananchi wote wa Zanzibar.

Awali akiongea na kutoa salamu kutoka FDH, Bwn Salali ameahidi kuhakikisha  taasisi yake kwa kushirikiana  na STAMICO  itahakikisha Nishati hii inafika kwenye  Magereza  yote kwa wingi na inafika katika ubora unaostahili.

Naye, Kamishna Khamis ameishukuru na kuipongeza STAMICO  kwa kuhakikisha Nishati hii inafika  Zanzibar.

Ameomba pia STAMICO  iangalie kuwapa fursa hii  ya kusambaza  Nishati hii kwa wale  wafungwa ambao wamemaliza vifungo vyao ili iwe njia ya kujitengenezea Kipato  baada ya kumaliza vifungo vyao.

Kamishna ametoa rai kwa taasisi nyingine kuhakikisha ziznaanza kutumia Nishati Safi kuendana na agenda ya kitaifa ya Nishati Safi ili kulinda mazingira.

Naye, Mwenyekiti  wa Wanawake na Samia Bi Fatuma Madidi ameipongeza STAMICO  kwa juhudi za kuhamasisha matumizi ya Nishati Safi na akapigia msumari kwenye suala la kuhakikisha na  taasisi yake hiyo inashiriki kikamilifu kuisambaza Nishati ya Rafiki Briquettes  katika kona zote za Tanzania.

STAMICO  imejipanga  kuhakikisha inaendelea  kuwa kinara katika kuhamasisha matumizi ya Nishati Safi Tanzania Nzima.





Na Farida Saidi Morogoro

Wanafunzi 6,800 kutoka nchi tano za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) wamewasili mkoani Morogoro kushiriki Mashindano ya Michezo ya Wanafunzi wa Shule za Msingi na Sekondari ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (FEASSA) 2026, yanayotarajiwa kuanza rasmi kesho, Agosti 12, hadi Agosti 23, mwaka huu.

Mashindano hayo, yanayofanyika kwa mara ya 23 katika Jumuiya ya Afrika Mashariki na mara ya tano nchini Tanzania, yatawakutanisha wanafunzi kutoka Tanzania, Kenya, Uganda, Rwanda na Burundi.

Akizungumza na waandishi wa habari mjini Morogoro, Mkuu wa Mkoa huo, Adam Kighoma Malima, amesema Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), imejipanga kuhakikisha mkoa huo unakuwa mwenyeji bora wa mashindano hayo.

Amesema jumla ya viwanja 21 pamoja na maeneo manane ya malazi vimetengwa kwa ajili ya washiriki wa mashindano hayo.

Malima amewahakikishia washiriki kuwa ulinzi na usalama umeimarishwa vya kutosha, huku akiwataka wananchi wa Morogoro kuchangamkia fursa za kiuchumi zitakazotokana na ujio wa maelfu ya wageni.

Aidha, amewataka wakazi wa mkoa huo kuwakaribisha wageni kwa ukarimu na kutumia mashindano hayo kujenga mahusiano mazuri kati ya Tanzania na nchi nyingine wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Amesema Tanzania itawakilishwa na wanafunzi 1,510 kutoka mikoa 26 ya Tanzania Bara, ikiwa ni idadi kubwa zaidi ya washiriki kutoka nchini humo katika historia ya mashindano hayo.

Kwa upande wa Morogoro, Malima amesema mkoa huo utashiriki katika michezo 13 baada ya kufanya vizuri katika mashindano ya UMISSETA na UMITASHUMTA yaliyofanyika mkoani Iringa Juni mwaka huu.

Kwa ujumla, FEASSA 2026 itahusisha michezo 20 kwa wanafunzi wa shule za sekondari, michezo sita kwa shule za msingi na michezo minne kwa wanafunzi wenye mahitaji maalum.

Malima amesema ujio wa maelfu ya washiriki na wageni unatoa fursa kubwa kwa wananchi kunufaika kiuchumi kupitia biashara, usafiri, chakula, malazi na huduma mbalimbali.

Ameongeza kuwa mashindano hayo pia yatatoa fursa ya kutangaza vivutio vya utalii vya Morogoro na Tanzania kwa ujumla kwa wageni kutoka nchi mbalimbali za Afrika Mashariki.

Ufunguzi rasmi wa mashindano hayo unatarajiwa kufanyika Agosti 16, ambapo Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, anatarajiwa kuwa mgeni rasmi.

Mkuu huyo wa Mkoa amewataka wananchi kujitokeza kwa wingi kushuhudia mashindano hayo na kuwakaribisha wageni kwa ukarimu, huku akivitaka vyombo vya habari kutumia fursa hiyo kuitangaza Morogoro na Tanzania kwa ujumla.

Madaktari bingwa wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) leo, Agosti 6, 2026, wamefanikiwa kufanya upasuaji wa kwanza wa kutenganisha mapacha walioungana aina ya parasitic conjoined twins, ambapo mmoja wa mapacha hakukua kikamilifu na alikuwa akimtegemea mwenzake kwa ukuaji na uhai.

Akizungumza mara baada ya upasuaji huo, Dkt. Victor Ngotta, Bingwa wa Upasuaji wa Watoto wa MNH, amesema mafanikio hayo yanaonyesha uwezo wa hospitali kushughulikia kesi ngumu na adimu zinazohitaji utaalamu wa hali ya juu, na ni hatua muhimu katika kuendelea kuimarisha huduma za upasuaji wa kibingwa nchini.

Dkt. Ngotta amesema upasuaji huo ulihitaji maandalizi ya kina na ushirikiano wa wataalamu kutoka fani mbalimbali kutokana na hali ya kipekee ya mtoto huyo, ambaye alikuwa na pacha aliyekuwa na mikono, miguu na sehemu ya kiuno pekee huku akimtegemea mwili wa mwenzake kwa ukuaji na uhai.

Mafanikio ya upasuaji huo yanaendelea kuimarisha nafasi ya Hospitali ya Taifa Muhimbili kama kituo kinachoongoza nchini katika utoaji wa huduma za kibingwa na ubingwa bobezi.

Mtoto anaendelea vizuri na yupo chini ya uangalizi wa karibu wa madaktari









Na Mwandishi Wetu
MAMLAKA ya Uwekezaji na Maeneo Maalum ya Kiuchumi Tanzania (TISEZA) na Vodacom Tanzania PLC zimesaini makubaliano ya ushirikiano yenye lengo la kuharakisha mageuzi ya kidijitali katika mfumo wa uwekezaji nchini na kuboresha huduma kwa wawekezaji wa ndani na nje ya Tanzania.

Ushirikiano huo wa miaka miwili umewekwa rasmi kupitia Mkataba wa Makubaliano (MoU) uliosainiwa jijini Dar es Salaam jana, ukilenga kutumia teknolojia katika kurahisisha huduma za uwekezaji, kuboresha mazingira ya kufanya biashara na kuimarisha Tanzania kama eneo linalovutia uwekezaji endelevu na wenye thamani kubwa.

Kupitia makubaliano hayo, Vodacom Tanzania itatoa huduma mbalimbali za teknolojia kwa TISEZA, zikiwemo mawasiliano ya kibiashara, huduma za intaneti, teknolojia ya Internet of Things (IoT) pamoja na huduma za fixed internet.

Huduma hizo zinatarajiwa kusaidia TISEZA katika utekelezaji wa jukumu lake la kukuza, kuratibu na kuwezesha uwekezaji nchini, huku zikiboresha uzoefu wa wawekezaji katika hatua mbalimbali za uwekezaji.

Mbali na huduma za kiteknolojia, taasisi hizo zitashirikiana katika kuandaa shughuli za kutangaza fursa za uwekezaji nchini, ikiwemo mikutano ya wafanyabiashara, roadshows na majukwaa ya kuwafikia na kuwahudumia wawekezaji.

Akizungumza wakati wa hafla ya kusaini makubaliano hayo leo Agosti 11, 2026, Mkurugenzi wa Biashara wa Vodacom Tanzania, Nguvu Kamando, amesema teknolojia imekuwa nyenzo muhimu katika kukuza uwekezaji, ubunifu na ushindani wa kiuchumi.

Amesema ushirikiano huo utaunganisha uwezo wa Vodacom katika teknolojia na jukumu la TISEZA la kukuza uwekezaji, kwa lengo la kujenga mazingira yaliyounganishwa zaidi, yenye ufanisi na rafiki kwa wawekezaji.

“Teknolojia imekuwa kichocheo muhimu cha uwekezaji, ubunifu na ushindani wa kiuchumi. Kupitia ushirikiano huu na TISEZA, tunaunganisha uwezo wa Vodacom katika teknolojia na dhamira ya Mamlaka ya kukuza uwekezaji,” amesema Kamando.

Amesema lengo ni kuhakikisha teknolojia inakuwa kichocheo cha uwekezaji kwa kuwezesha wafanyabiashara kupata mawasiliano na suluhisho za kidijitali zitakazowasaidia kuanzisha shughuli zao kwa haraka, kufanya kazi kwa ufanisi na kuchangia katika ukuaji wa uchumi wa Tanzania.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa TISEZA, Gilead J. Teri, amesema ushirikiano huo unaonyesha dhamira ya pamoja ya taasisi hizo katika kuboresha huduma kwa wawekezaji na kuendana na mwelekeo wa Tanzania wa kujenga uchumi unaotegemea ubunifu na teknolojia.

Amesema Dira ya Maendeleo ya Tanzania 2050 inasisitiza umuhimu wa kuwa na uchumi wenye ushindani, unaoongozwa na ubunifu na unaoungwa mkono na miundombinu ya kisasa ya kidijitali pamoja na huduma bora za umma.

“Ushirikiano huu unaonyesha dhamira yetu ya pamoja ya kutumia teknolojia kuboresha uzoefu wa wawekezaji, kuimarisha uwezeshaji wa uwekezaji na kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma,” amesema Teri.

Ameongeza kuwa kadiri Tanzania inavyoendelea kuvutia uwekezaji wa kimkakati katika sekta mbalimbali, ushirikiano na Vodacom utasaidia kuiweka nchi katika nafasi nzuri zaidi ya kuwa eneo linalopendelewa kwa uwekezaji endelevu na wenye thamani kubwa.

Ushirikiano huo pia unaendana na vipaumbele vya maendeleo ya taifa vya kuimarisha ushirikiano kati ya sekta ya umma na binafsi, pamoja na kutumia teknolojia za kidijitali kuboresha mfumo wa uwekezaji nchini.

Kupitia kuboresha mawasiliano, kuchochea ubunifu wa kidijitali na kuimarisha huduma zinazolenga wawekezaji, ushirikiano huo unatarajiwa kujenga mazingira ya uwekezaji yenye ufanisi, ushindani na yanayotumia teknolojia.

Vodacom Tanzania, ambayo ni miongoni mwa kampuni zinazoongoza katika teknolojia na mawasiliano nchini, imeendelea kuwekeza katika miundombinu ya kidijitali na suluhisho za kiteknolojia kwa ajili ya biashara, taasisi na jamii.

Ushirikiano huo na TISEZA unaelezwa kuwa sehemu ya jitihada za kampuni hiyo kuunga mkono ajenda ya Tanzania ya mageuzi ya kidijitali na kujenga mazingira yanayowezesha ubunifu, uwekezaji na ukuaji endelevu wa uchumi.



Na Mwandishi Wetu.
GLOBAL Education Link (GEL) imewakabidhi nyaraka rasmi za safari wanafunzi 387 wa Kitanzania wanaotarajia kwenda kuendelea na masomo ya elimu ya juu nchini China na India, huku wakihimizwa kutumia fursa hiyo kujenga maarifa, ujuzi, teknolojia, mitandao ya kimataifa na uwezo wa kujitengenezea fursa za maisha, badala ya kulenga shahada pekee.

Ukabidhi huo umefanyika kupitia mikutano miwili maalumu iliyofanyika Agosti 10 na 11, 2026 katika Ukumbi Mkuu wa Makao Makuu ya Global Education Link, Dar es Salaam, na kuhudhuriwa na wazazi pamoja na walezi wa wanafunzi hao.

Kati ya wanafunzi hao, 198 wanaelekea China na 189 India kwa ajili ya kuanza masomo katika vyuo mbalimbali vya elimu ya juu.

Lengo la mikutano hiyo lilikuwa kuwakabidhi wanafunzi nyaraka muhimu za safari zilizokamilishwa na GEL, zikiwemo pasipoti, visa, tiketi za ndege, NOC (No Objection Certificate), cheti au kijitabu cha chanjo ya homa ya manjano (Yellow Fever Certificate) pamoja na nyaraka nyingine zinazohitajika na mamlaka husika kulingana na nchi, chuo na masharti ya safari.

Mbali na kukabidhiwa nyaraka hizo, wanafunzi pamoja na wazazi na walezi wao walipata maelekezo ya mwisho kuhusu taratibu za safari, uhamiaji, mazingira ya vyuo, makazi, bima ya afya, usalama, matumizi ya fedha, nidhamu na namna ya kukabiliana na mazingira mapya watakapofika katika nchi wanazokwenda.

Mtoa mada mkuu katika mikutano hiyo alikuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Global Education Link, Abdulmalik Mollel, akishirikiana na wawakilishi wa vyuo kutoka China na India waliotoa ufafanuzi kuhusu masomo, huduma za vyuo na maisha ya mwanafunzi wa kimataifa.

Akizungumza katika mikutano hiyo, Mollel aliwataka wanafunzi kutokwenda China na India kwa lengo la kupata cheti au shahada pekee, bali kutumia mazingira ya vyuo watakakosoma kujenga uwezo mpana utakaowasaidia baada ya kuhitimu.

Alisema kwenda kusoma nje ya nchi kunamfungulia mwanafunzi mazingira mapya yenye teknolojia, maabara, warsha, vituo vya ubunifu, wataalamu pamoja na wanafunzi kutoka mataifa mbalimbali, hivyo ni jukumu la mwanafunzi kutumia fursa hizo kwa manufaa yake na Taifa.

Aliwataka vijana hao kwenda zaidi ya masomo ya darasani kwa kutembelea maabara, warsha na vituo vya ubunifu na kujifunza kwa vitendo namna teknolojia na bidhaa mbalimbali zinavyozalishwa na kutumika katika kutatua changamoto za jamii.

Akitolea mfano mwanafunzi anayesomea Business Administration, alisema haipaswi kutosha kujifunza nadharia za usimamizi wa biashara pekee, bali anapaswa kutafuta maarifa kuhusu bidhaa, teknolojia, uzalishaji na mifumo mbalimbali ya viwanda ili aweze kuelewa kile anachoweza kukisimamia au kukigeuza kuwa biashara.



 Na: Calvin Gwabara – Dodoma.

Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria (OCPD) imeendelea kuwekeza katika kuwaendeleza watumishi wake kitaaluma kwa kuwapatia fursa za mafunzo ndani na nje ya nchi, hatua inayolenga kuongeza idadi ya wataalamu wenye weledi, utaalamu wa kisekta na uwezo wa kuandaa sheria bora zinazowezesha utekelezaji wa sera na mipango ya Serikali.

Mwandishi Mkuu wa Sheria (CPD) Bwana Onorius John Njole wakati akiongea na Mwandishi wetu kuhusu mpango huo wa mafunzo.

Hayo yamebainishwa na Mwandishi Mkuu wa Sheria (CPD) Bwana Onorius John Njole wakati akiongea na Mwandishi wetu kuhusu jitihada zinazochukuliwa na ofisi yake katika kuiwezesha nchi kupata sheria bora zinazokwenda na wakati.

Bwana Njole amesema Uandishi wa Sheria ni taaluma maalumu yenye misingi, kanuni na viwango vyake, hivyo inahitaji mafunzo mahsusi na uwekezaji endelevu katika kujenga uwezo wa wataalamu.

“Ingawa Waandishi wa Sheria ni Wanasheria, si kila Mwanasheria ni Mwandishi wa Sheria mtu anakuwa Mwandishi wa Sheria baada ya kupata taaluma maalumu ya uandishi wa Sheria,” amesema Njole.

Amesema mkakati wa Ofisi hiyo haujajikita katika kuwafundisha waandishi namna ya kuandika sheria pekee bali pia kuwajengea utaalamu katika sekta ambazo sheria wanazoandika zinalenga kuzisimamia kwa kuwa uelewa huo huwasaidia kutambua mahitaji halisi ya sekta na kuandaa sheria zinazoweza kutatua changamoto na kuwezesha utekelezaji wa mipango ya Taifa.

Mwandishi huyo Mkuu wa Sheria amesema kwa kutambua umuhimu wa taaluma hiyo, Ofisi ya Mwadishi Mkuu wa Sheria (OCPD) imekuwa ikiwapeleka watumishi kupata mafunzo katika vyuo na taasisi mbalimbali ndani na nje ya nchi zilizobobea, huku baadhi wakipata utaalamu katika maeneo mahsusi kama Kodi, Sheria za Bahari na Uandishi wa Sheria.

Aidha amesema kuwa OCPD pia imeweka mkazo katika mafunzo ya ndani kwa kuwa sehemu kubwa ya uandishi wa sheria hujifunzwa kupitia utekelezaji wa majukumu ya kila siku. Ofisi hiyo imekuwa na mfumo wa kufundishana baina ya waandishi wa sheria, ikiwemo madarasa ya maeneo mbalimbali ya uandishi wa sheria yanayofanyika kila Jumatatu.

“Katika mwaka uliomalizika, Waandishi wawili walipelekwa Chuo cha West Indies, wengine tisa Chuo cha Sheria cha Zambia kwa ajili ya mafunzo ya uandishi wa sheria, huku mpango wa mwaka 2026 ukilenga kupeleka waandishi wengine wawili Zambia na wawili katika Chuo cha Sheria cha London” alieleza Njole.

Aliongeza “Uwekezaji huu pia unalenga kuwa na wataalamu wenye utaalamu wa kisekta, ambapo katika mwaka uliomalizika waandishi wawili walipata shahada za uzamili katika eneo la kodi, huku waandishi wanne wakipata shahada za uzamili katika Sheria za Bahari nchini Malta”.

Mwandishi huyo Mkuu wa Sheria alisema lengo la muda mrefu ni kuhakikisha Tanzania inakuwa na wataalamu wa kutosha katika uandishi wa sheria wenye uwezo wa kukidhi mahitaji ya ndani na pia kutoa huduma za uandishi wa sheria katika nchi nyingine, hususan ndani ya Jumuiya ya Madola.

Miongoni mwa wanufaika wa mpango huo ni Boniphas Mondu Giabe aliyepata fursa ya kusoma Shahada ya Uzamili katika Uandishi wa Sheria katika Chuo Kikuu cha West Indies, Kampasi ya Cave Hill, nchini Barbados ambaye amesema mafunzo hayo yamemsaidia kuongeza ujuzi katika Uandishi wa Sheria na kumjengea uelewa wa umuhimu wa kuandaa sheria kwa lugha inayoeleweka kwa urahisi na inayozingatia misingi ya kikatiba na haki za binadamu.

Baadhi ya Watumishi wa Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria wakiwa kwenye picha ya pamoja mara baada ya mahafali yaliyofanyika katika Chuo cha Kimataifa cha Sheria za Baharini (IMO International Maritime Law Institute – IMLI), nchini Malta.

“Moja ya mambo muhimu niliyojifunza ni kwamba sheria zinapaswa kuandikwa kwa lugha na mtindo unaowawezesha watumiaji kuzielewa kwa urahisi lakini pia zinapaswa kuzingatia misingi ya kikatiba pamoja na haki za binadamu,” amesema Giabe.

Amesema maarifa aliyoyapata katika maeneo ya sheria za utawala, sheria za katiba, mafuta na gesi yanaendelea kumsaidia katika utekelezaji wa majukumu yake, huku akishirikisha ujuzi huo na waandishi wengine wa sheria katika kuandaa sheria bora na zinazotabirika.

Nae mnufaika mwingine Bi. Loveness Jacob aliyepata ufadhili wa Shahada ya Uzamili katika Sheria za Kimataifa za Baharini kutoka Chuo cha Kimataifa cha Sheria za Baharini (IMO International Maritime Law Institute – IMLI), nchini Malta, ambapo amesema mafunzo hayo yamemwongezea utaalamu katika eneo muhimu la kimkakati kwa Serikali na Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria.

“Utaalamu nilioupata utasaidia katika uandaaji wa Sheria zinazotokana na mikataba ya kimataifa ya baharini, uandaaji wa nyaraka za utekelezaji wa mikataba hiyo na kuimarisha usimamizi wa masuala ya bahari na kuchangia katika kukuza uchumi wa buluu kupitia uandishi wa sheria za sekta hiyo, alisema Jacob.

Amesema mafunzo hayo pia yamempa fursa ya kupata uzoefu wa vitendo katika masuala ya sheria za kimataifa kupitia ushiriki katika mkutano wa Kamati ya Kisheria ya Shirika la Kimataifa la Bahari (IMO Legal Committee) ambapo alijifunza namna nchi zinavyoshiriki katika mijadala ya kimataifa na kuwasilisha hoja za kisheria.

Aidha kwa upande wake Bi. Winfrida Mwera ambaye ni Kaimu Mkurugenzi Msaidizi wa Uandishi na Ufasiri wa Sheria Ndogo katika OCPD, aliyepata fursa ya kusoma Postgraduate Diploma in Legislative Drafting, kwa lengo la kuimarisha uwezo wake katika kuandaa na kurekebisha miswada ya sheria, amesema mafunzo hayo yamemwongezea ujuzi katika matumizi ya mbinu na misingi mbalimbali ya uandishi wa sheria, pamoja na uwezo wa kuandaa sheria zilizo wazi, sahihi na zenye ufanisi.

“Nitatumia ujuzi na maarifa niliyoyapata kupitia mafunzo haya katika kuandaa rasimu za sheria zenye ubora wa juu, kupunguza mapungufu katika uandishi wa sheria na kutoa mchango wenye tija katika utekelezaji wa majukumu ya kila siku ya OCPD,” amesema Mwera.

Amesema uwekezaji huo umechangia kuongeza uwezo wa watumishi na kuboresha utendaji wa taasisi huku akitoa wito wa kuendelea kutolewa kwa fursa za mafunzo kwa wataalamu wengine.

Katika kuhakikisha mafunzo wanayoyapata kutoka ndani na nje ya nchi Ofisi hiyo ina siku maalumu kila wiki kwa wahitimu kukutana na watumishi wenzao na kuwafndisha na kujengeana uwezo kupitia mafunzo ya ndani ili wote wanufaike na kuchangia ubora wa kazi za ofisi kwa maslahi mapana ya Taifa.

Mwandishi wa Sheria kutoka Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria chini akifurahia mara baada ya kupokea tuzo kwa kufanya vizuri zaidi kwenye eneo la Sheria za Bahari wakati wa mahafali kutoka Chuo cha Kimataifa cha Sheria za Baharini (IMO) nchini Malta.  

m



 


Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe. Hamza S. Johari amewasilisha Maelezo ya Serikali kuhusu Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na.2) wa Mwaka 2026 (The Written Laws (Miscellaneous Amendments ) (No.2)  Bill, 2026 kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria tarehe 11 Agosti, 2026 Bungeni Jijini, Dodoma.


Aidha,  Mhe. Johari ametoa maelezo ya Serikali kuhusiana na  Muswada huo unaolenga kufanya marekebisho katika Sheria kama vile Sheria ya Mipango ya Matumizi ya Ardhi, Sura ya 166, Sheria ya Serikali za Mitaa (Mamlaka ya Wilaya) Sura ya 287, Sheria ya Serikali za Mitaa (Mamlaka za Miji), Sura ya 288, Sheria ya Baraza la Usalama la Taifa, Sura ya 61, Sheria ya Uthamini na Usajili wa Wathamini, Sura ya 138 na Sheria ya Uhifadhi wa Wanyamapori, Sura ya 283.


Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria inayoongozwa na Mwenyekiti Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro (Mb) imepokea na kujadili maelezo Serikali kuhusiana na Muswada huo.






Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
MAMLAKA ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) imetakiwa kushirikiana na kiwanda cha kutengeneza samani za ndani cha EDOSAMA, kilichopo Kinyerezi, Dar es Salaam, katika kuandaa Watanzania wengi zaidi wenye ujuzi na umahiri katika fani ya useremala ili kukidhi mahitaji ya soko la ajira ndani na nje ya nchi.

Wito huo umetolewa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Hussein Mohamed Omar, wakati wa ziara katika karakana za kiwanda hicho kwa lengo la kujionea namna shughuli za useremala zinavyoendeshwa pamoja na matumizi ya mashine na teknolojia za kisasa katika utengenezaji wa samani mbalimbali.

Akizungumza na viongozi wa VETA na EDOSAMA wakati wa ziara hiyo, Dkt. Omar amesema moja ya matakwa ya Serikali ya Awamu ya Sita ni kukuza ushirikiano kati ya waajiri, wenye viwanda na vyuo vya elimu na mafunzo, ili kuhakikisha vijana wanapata ujuzi unaowawezesha kujiajiri, kuajiriwa na kuajiri wengine, sambamba na kukidhi mahitaji ya soko la ajira.

Amesema ushirikiano kati ya VETA na EDOSAMA utakuwa na umuhimu mkubwa katika kuzalisha vijana wenye uwezo na weledi wa kushindana katika soko la ajira, hususan katika sekta ya utengenezaji wa samani.

“Na sisi kama Wizara ya Elimu na wasimamizi wakuu wa mpango huo, tumeona umuhimu wa ushirikiano kati ya VETA yenye jukumu la kuzalisha vijana kupitia utoaji wa mafunzo ya ufundi stadi na EDOSAMA kama kituo cha uandaaji mafundi mahiri katika eneo la utengenezaji wa samani,” amesema Dkt. Omar.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa VETA, CPA Kasore, amemshukuru Naibu Katibu Mkuu kwa ziara hiyo na kueleza kuwa Februari 2026, Serikali kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ilizindua mpango wa ushirikiano baina ya waajiri, wenye viwanda na vyuo vinavyotoa elimu na mafunzo ya ufundi stadi.

Amesema mpango huo unalenga kuhakikisha Watanzania, hasa vijana, wanapatiwa ujuzi unaohitajika katika soko la ajira na hivyo kuchangia kufikiwa kwa malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

“Jukumu letu VETA ni kuhakikisha tunayaishi maono ya Serikali ya Awamu ya Sita kwa kutoa mafunzo yatakayowapa Watanzania ujuzi na kuwaandaa kushindana katika soko la ajira na kukidhi mahitaji ya wenye viwanda, waajiri na mabadiliko ya teknolojia,” amesema CPA Kasore.

Ameongeza kuwa ushirikiano na EDOSAMA utawezesha kuandaa mitaala inayoendana na mahitaji ya soko la ajira, kuwaandaa wakufunzi wenye uwezo wa kuwapatia vijana ujuzi unaohitajika sokoni, pamoja na kuboresha karakana, mitambo na mashine zinazotumika katika kujifunzia na kufundishia.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa EDOSAMA, Edward Saguda, amesema sekta ya misitu bado ina mchango mdogo katika uchumi wa nchi, ikiwa inachangia asilimia 3.5 ya Pato la Taifa, licha ya kuwa na uwezo mkubwa wa kuongeza mapato na ajira.

Saguda amesema iwapo sekta hiyo itaangaliwa kwa mtazamo mpana zaidi na Serikali, inaweza kuongeza mchango wake hadi zaidi ya asilimia 10 ya mapato ya Serikali na kutengeneza ajira nyingi zaidi kwa Watanzania.

Ameiomba VETA kuharakisha kuanzisha ushirikiano rasmi na EDOSAMA ili kusaidia Serikali na Watanzania kunufaika zaidi na fursa zilizopo katika sekta ya misitu na utengenezaji wa samani





Na Mwandishi Wetu
SHIRIKA la Mawasiliano Tanzania (TTCL) limeibuka kinara katika utoaji wa huduma bora za mawasiliano nchini, huku likieleza kuwa litaendelea kuwekeza katika miundombinu na mifumo ya huduma kwa wateja ili kuongeza ufanisi.

Taarifa hiyo imetolewa katika ripoti ya robo mwaka iliyosomwa na Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Angela Kairuki, ikieleza hatua mbalimbali zilizochukuliwa katika kuboresha huduma za mawasiliano nchini.

Akizungumza kuhusu maboresho hayo, Mkurugenzi Mkuu wa TTCL, Mbanguka, amesema uwekezaji katika miundombinu na mifumo umeiwezesha kampuni hiyo kuendelea kutoa huduma bora kwa wananchi, huku ikiimarisha mifumo inayorahisisha huduma kwa wateja kwa ufanisi na gharama nafuu.

“TTCL imekuwa kinara katika utoaji wa huduma bora za mawasiliano. Haya yote yanawezekana kutokana na miundombinu ambayo tumeiboresha zaidi, lakini pia uwekezaji katika mifumo ya ndani na mifumo ya nje ya namna ya kuwahudumia wateja wetu kwa urahisi na unafuu zaidi,” amesema.

Amesema TTCL itaendelea kuboresha miundombinu yake ili kuhakikisha huduma za mawasiliano zinawafikia wananchi katika maeneo mbalimbali nchini, sambamba na kuimarisha mifumo ya huduma kwa wateja.

Mbanguka amesema maboresho hayo yataendelea kutekelezwa kwa kuhakikisha mifumo inayosaidia utoaji wa huduma inawekwa na kukamilishwa kwa wakati, ili shirika hilo liendelee kutoa huduma bora, za haraka na zenye ufanisi.

Ameongeza kuwa hatua hiyo ni sehemu ya juhudi za TTCL katika kuimarisha huduma za mawasiliano nchini, huku ikilenga kukidhi mahitaji yanayoongezeka ya wananchi na taasisi katika matumizi ya teknolojia na huduma za kidijitali.

Katibu wa Tume ya Utumishi wa Umma, Nolasco Kipanda, akifungua mafunzo ya usalama na afya mahali pa kazi kwa wakaguzi wa Tume hiyo yaliyoandaliwa na Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA) kwa lengo la kuwajengea uelewa wakaguzi hao wenye jukumu la kukagua uzingatiaji wa sheria na miongozo mbalimbali katika sekta ya umma.
Mkurugenzi wa Mafunzo, Tafiti, Takwimu na Uhamasishaji wa OSHA, Bw. Joshua Matiko, akitoa ufafanuzi wa hoja mbalimbali zilizoibuliwa na washiriki katika mafunzo ya usalama na afya mahali pa kazi kwa Wakaguzi wa Tume ya Utumishi wa Umma yaliyoandaliwa na Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA).
Katibu wa Tume ya Utumishi wa Umma, Nolasco Kipanda (Katikati) akiwa na viongozi wenzake wakifuatilia mafunzo ya usalama na afya mahali pa kazi yaliyotolewa na OSHA kwa Wakaguzi wa Tume hiyo.
Meneja Mafunzo wa OSHA, Mhandisi Shaban Mkindi, akiwasilisha mada katika mafunzo ya usalama na afya mahali pa kazi kwa Wakaguzi wa Tume ya Utumishi wa Umma yaliyoandaliwa na Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA).
Wakaguzi wa Tume ya Utumishi wa Umma wakifuatilia mada mbalimbali katika mafunzo yaliyoandaliwa na Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA) kwa lengo la kuwajengea uelewa juu ya masuala ya usalama na afya mahali pa kazi.
Afisa Mafunzo Mwandamizi wa OSHA, Bw. Simon Lwaho, akiwasilisha mada katika mafunzo ya usalama na afya mahali pa kazi kwa Wakaguzi wa Tume ya Utumishi wa Umma yaliyoandaliwa na Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA).

Na Mwandishi Wetu
TUME ya Utumishi wa Umma imesema serikali ina nia ya dhati ya kuhakikisha watumishi wa umma wanakuwa salama na wenye afya njema na hivyo kutekeleza wajibu wao wa kuwahudumia wananchi ipasavyo.

Kauli hiyo imeelezwa na Katibu wa Tume ya Utumishi wa Umma, Nolasco Kipanda, alipofungua mafunzo ya usalama na afya mahali pa kazi kwa wakaguzi wa Tume hiyo yaliyoandaliwa na Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA) kwa lengo la kuwajengea uelewa wakaguzi hao wenye jukumu la kukagua uzingatiaji wa sheria na miongozo mbalimbali katika sekta ya umma.

Amesema serikali inatamani kuona kila mtumishi wa umma anakuwa salama dhidi ya ajali na magonjwa yatokanayo na kazi ili aweze kutoa mchango wake kikamilifu katika kutekeleza majukumu ya serikali.

“Sote tunafahamu kwamba kinga ni bora kuliko tiba, Sheria ya Afya na Usalama Mahali pa Kazi inaelekeza maeneo yote ya kazi kuwa na mifumo madhubuti ya kuwalinda wafanyakazi dhidi ajali na magonjwa yatokanayo na kazi. Serikali inaamini kwamba watumishi wakiwa na afya njema, utendaji wao utaimarika na tayari ina chombo chake mahsusi cha kusimamia hilo ambacho ni Taasisi ya OSHA,” ameeleza Katibu wa Tume.

Amebainisha kwamba si wajibu wa Tume kusimamia utekelezaji wa Sheria bali Tume hiyo ina jukumu la kuhakikisha waajiri wanatekeleza sheria hiyo pamoja na miongozo mingine inayotolewa na OSHA ili kulinda afya na usalama wa watumishi wa serikali.

“Kutokana na umuhimu wa rasilimali watu, Serikali kupitia Ofisi ya Rais- Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora ilisisitiza Tume kufanya ukaguzi wa uzingatiaji wa sheria ya usalama na afya mahali pa kazi ili kuhakikisha watumishi wa umma wanafanya kazi katika mazingira bora na hivyo kuwa na ufanisi,” amesisitiza Katibu Kipanda.

Aidha, amewataka wakaguzi wa Tume kuwa na uelewa wa kina kuhusu Sheria ya Usalama na Afya mahali pa kazi ili waweze kufanya tathmini sahihi ya utekelezaji wa sheria hiyo na kushauri maboresho stahiki.

Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa OSHA, Bi. Khadija Mwenda, ameipongeza serikali kwa kudhihirisha nia ya dhati ya kuwalinda watumishi dhidi ya ajali na magonjwa yatokanayo na kazi kupitia utekeleza wa sheria na miongozo ya usalama na afya mahali pa kazi.

"Napenda kutoa shukrani zangu kwa Rais, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuonesha nia ya dhati ya kuhakikisha kwamba nguvukazi ya nchi inalindwa katika sekta zote za umma na binafsi ambapo kupitia maelekezo yake masuala ya usalama na afya yamejumuishwa katika kanuni za kudumu za utumishi wa umma,” amesema Mwenda na kuongeza:

“Tunaishukuru Tume kwa kutushirikisha ambapo tumeweza kuandaa mafunzo ya kuwajengea uelewa wakaguzi wake ili wakienda kukagua wajue ni maeneo gani muhimu ya kuyafuatilia na wametuahidi baada ya ukaguzi tutakuwa na kikao cha pamoja kwa ajili ya kupata mrejesho.”
Baadhi ya Wakaguzi wa Tume wameyaelezea mafunzo hayo kama nyenzo muhimu katika utekelezaji wa majukumu yao.

“Mafunzo haya yametupa uelewa mpana sisi kama wakaguzi utakaotuwezesha kutekeleza majukumu yetu kwa ufanisi,” ameeleza Rose Silayo. 

“Kipekee ninashukuru kwa mafunzo haya ambayo yatatuwezesha kukagua na kushauri ipasavyo uzingatiaji wa masuala ya usalama na afya ili kulinda afya za watumishi wa umma,” ameeleza David Shombe.
Mwaka 2022, Tume ilifanya maboresho ya mfumo wa ukaguzi wa masuala ya kiutumishi ili kuendana na sera, sheria na mazingira ya wakati husika ambapo maeneo sita ya kiutawala yaliongezwa katika maeneo saba yaliyokuwa yakikaguliwa awali. Eneo la usalama na afya kazini ni miongoni mwa maeneo yaliyoongezwa.

Na Janeth Raphael - MichuziTv 

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, amewataka wananchi wanaomiliki silaha kuhakikisha wanakamilisha taratibu zote za kisheria na vibali vinavyohitajika kabla ya Agosti 30, 2026, akieleza kuwa operesheni maalum ya ukaguzi wa silaha itaanza mara baada ya muda huo.

Chalamila ametoa agizo hilo wakati akizungumza na waandishi wa habari leo , akisisitiza kuwa wamiliki ambao kwa sababu mbalimbali, ikiwemo kusahau au kutokuwa na uelewa wa kutosha kuhusu taratibu, hawajakamilisha malipo ya vibali au hatua nyingine za kisheria, wanapaswa kutumia muda uliopo kufika katika mamlaka husika na kurekebisha hali hiyo.

Amesema hatua hiyo inalenga kuhakikisha silaha zinazomilikiwa na wananchi katika Mkoa wa Dar es Salaam zinakuwa na kumbukumbu na vibali halali vinavyotambulika kisheria, kabla ya kuanza kwa operesheni hiyo.

Kwa upande mwingine, Mkuu huyo wa Mkoa amewataka watu wanaomiliki silaha bila kufuata sheria kuzisalimisha kwa hiari katika Jeshi la Polisi au kituo cha Polisi kilicho karibu kabla ya operesheni kuanza. Amesisitiza kuwa hatua hiyo inaweza kusaidia wahusika kuepuka kukumbana na hatua za kisheria zitakazochukuliwa baada ya ukaguzi kuanza.

Aidha, Chalamila ametoa mwito kwa familia ambazo ndugu zao wamefariki huku wakiacha silaha zenye vibali halali kuhakikisha hazizifichi wala kuzihamisha bila kufuata utaratibu. Badala yake, amewataka kuwasilisha taarifa pamoja na silaha hizo kwa mamlaka husika ili kupata maelekezo ya kisheria kuhusu namna ya kushughulikia umiliki huo.

Kuhusu silaha zinazoripotiwa kuibiwa, amewataka wamiliki kutoa taarifa Polisi na kufuata taratibu zote zinazohitajika. Amesisitiza kuwa silaha hizo zinapopatikana, wahusika hawapaswi kuzificha au kuendelea kuzitumia bila kufuata maelekezo ya mamlaka.

Chalamila amesisitiza kuwa Agosti 30, 2026 ndiyo mwisho wa muda uliotolewa kwa wamiliki kuhakikisha wanakamilisha taratibu zao, akieleza kuwa baada ya tarehe hiyo operesheni maalum ya ukaguzi itaanza na yeyote atakayebainika kumiliki silaha kinyume cha sheria atachukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria.

Amewataka wananchi kutotumia muda uliobaki kupuuza agizo hilo, bali kuhakikisha mapema kuwa umiliki wa silaha zao uko katika hali halali na unaotambulika na mamlaka, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha udhibiti na usalama wa silaha katika Mkoa wa Dar es Salaam.






Na Mwandishi Wetu
WATANZANIA wameanza kunufaika na huduma za matibabu ya kibingwa zinazopatikana nchini, hali inayopunguza gharama na ulazima wa kusafiri nje ya nchi kutafuta matibabu.

Mkurugenzi Mtendaji wa Universal Medical Tourism, Dkt. Sharif Mollel, amesema huduma hizo zinapatikana katika Hospitali ya SINO iliyopo Mikocheni, Dar es Salaam.

Amesema kampuni yake inashirikiana na hospitali hiyo kurahisisha upatikanaji wa huduma za kibingwa, teknolojia za kisasa za matibabu pamoja na baadhi ya huduma za tiba za jadi za China, zinazojulikana kama Traditional Chinese Medicine. Amesema uwepo wa huduma hizo nchini unawapa Watanzania nafasi ya kupata matibabu bila kuingia gharama za tiketi za ndege, malazi, visa na matumizi mengine yanayotokana na safari za matibabu nje ya nchi.

“Lengo letu ni kuona Watanzania wanapata huduma nyingi zaidi hapa nchini. Kama huduma inayohitajika inapatikana Tanzania, hakuna sababu ya mgonjwa kuanza na safari ya kwenda nje ya nchi,” amesema.

Amesema baadhi ya wagonjwa kutoka nchi za Afrika Mashariki na ukanda wa SADC pia wameanza kuja Tanzania kupata huduma katika hospitali hiyo. Kwa mujibu wa Dkt. Mollel, hatua hiyo inaonesha kuwa Tanzania ina nafasi ya kujijenga kuwa kituo muhimu cha huduma za afya na medical tourism katika ukanda wa Afrika.

“Tunataka kuona medical tourism ikienda pande zote. Siyo Watanzania kwenda nje kutibiwa pekee, bali pia wagonjwa kutoka nchi nyingine kuja Tanzania kupata huduma,” amesema.

Amesema Hospitali ya SINO inatoa huduma mbalimbali za uchunguzi na matibabu kwa kutumia teknolojia za kisasa, zikiwemo huduma za mifupa na viungo, mgongo, mfumo wa neva, urology na physiotherapy. Hospitali hiyo pia ina teknolojia za uchunguzi zikiwemo Ultrasound, CT Scan na MRI, zinazosaidia madaktari kufanya uchunguzi wa kina kabla ya kuamua aina ya matibabu anayohitaji mgonjwa.

Mbali na tiba za kisasa, amesema Hospitali ya SINO inatoa baadhi ya huduma za Traditional Chinese Medicine, ikiwemo acupuncture, inayotumia sindano maalumu katika maeneo mahususi ya mwili chini ya usimamizi wa wataalamu. Amesema huduma hizo zinaweza kusaidia katika usimamizi wa baadhi ya hali za maumivu, misuli na viungo baada ya mgonjwa kufanyiwa tathmini ya kitaalamu.

Dkt. Mollel amesisitiza kuwa huduma za tiba za jadi za China hazikusudii kuchukua nafasi ya tiba za kisasa, bali hutolewa kulingana na ushauri na tathmini ya wataalamu. Ametoa wito kwa Watanzania, hususan wakazi wa Dar es Salaam, kutumia nafasi ya kuwepo kwa huduma hizo nchini kabla ya kufanya uamuzi wa kusafiri nje ya nchi kutafuta matibabu.

Dkt. Mollel amesema moja ya malengo ya Universal Medical Tourism ni kuendelea kuvutia wataalamu, teknolojia na uwekezaji wa afya kutoka nje ya nchi ili huduma nyingi zaidi zipatikane Tanzania. Amesema kampuni hiyo pia inalenga kuendeleza ushirikiano kati ya madaktari wa Tanzania na wataalamu kutoka China kupitia kambi za matibabu na programu mbalimbali za kubadilishana ujuzi.

“Tunapotengeneza mazingira ya daktari wa Tanzania kufanya kazi pamoja na mtaalamu kutoka China, tunamhudumia mgonjwa lakini pia tunajenga uwezo wa wataalamu wetu,” amesema. Amesema hatua hiyo inaweza kusaidia teknolojia na maarifa yanayoletwa nchini kubaki na kutumika kwa muda mrefu badala ya huduma kutegemea wataalamu wa nje pekee.

Dkt. Mollel amesema dhamira ya muda mrefu ni kuona Tanzania inapunguza idadi ya wagonjwa wanaolazimika kusafiri nje kwa huduma zinazoweza kutolewa nchini, huku ikiongeza idadi ya wagonjwa kutoka mataifa mengine wanaokuja kupata matibabu hapa nchini.

 

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amewasili Zanzibar, leo tarehe 11 Agosti 2026. Makamu wa Rais anatarajiwa kuwa Mgeni Rasmi katika Ufunguzi wa Jengo la Dakhalia katika Skuli ya Sekondari ya Hasnuu Makame – Kibuteni Unguja, ikiwa ni shamrashamra ya Tamasha la Kizimkazi. (Kizimkazi Festival 2026)



Top News