Na Ssgt Mawazo Mtondo - MWANZA.

MKUU wa Sehemu ya Michezo na Utamaduni katika Jeshi la Magereza, Kamishna Msaidizi wa Magereza (ACP) Solomon Mwambingu, LEO 19 Septemba, 2026, ameeleza maandalizi na mikakati ya Jeshi la Magereza kuelekea Mashindano ya Baraza la Michezo ya Majeshi Tanzania (BAMMATA) 2026.

ACP Mwambingu ameyasema hayo wakati akizungumza na Vyombo vya habari katika Ukumbi wa Mikutano wa Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustino (SAUT), jijini Mwanza, ambapo amesema Jeshi la Magereza Tanzania limejiandaa vyema katika michezo mbalimbali kuelekea mashindano hayo yanayotarajiwa kufanyika kuanzia Septemba 21 hadi Oktoba 5, 2026, katika Viwanja mbalimbali, jijini Mwanza.

Amesema kama sehemu ya maandalizi, Jeshi la Magereza lilifanya Mashindano ya CGP CUP jijini Dar es Salaam mwezi Agosti 2026, kwa lengo la kuziandaa timu na kuhakikisha zinafikia kiwango kizuri cha ushindani kuelekea BAMMATA.

“Jeshi la Magereza limejiandaa vyema katika michezo mbalimbali. Tunaendelea kuibua na kukuza vipaji, ambapo Kocha wa Timu ya Taifa ya Netiboli anatoka Jeshi la Magereza, pamoja na kuwa na wachezaji wanaowakilisha timu za taifa. Tumejiandaa vyema na tupo tayari kushindania vikombe katika BAMMATA 2026,” amesema ACP Mwambingu.

Aidha, ACP Mwambingu aliendelea kueleza kuwa ufunguzi na ufungaji wa Mashindano hayo utafanyika katika Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza, pia alitaja Viwanja vingine vitakavyotumika kwa ajili ya mashindano hayo pamoja na michezo husika itakayofanyika, alisema Uwanja wa CCM Kirumba utatumika wa michezo ya Mpira wa Pete (Netball), Riadha na Mpira wa Miguu (Football), pamoja na kufanyika kwa shughuli za ufunguzi na ufungaji wa mashindano. 

Uwanja wa Chuo cha Ualimu Butimba kutafanyika michezo ya Mpira wa Miguu (Football), Mpira wa Pete (Netball) na Mpira wa Kikapu (Basketball). 

Viwanja vya Milongo kutafanyika michezo ya Mpira wa Mikono (Handball), Mpira wa Kikapu (Basketball) na Mpira wa Wavu (Volleyball). Viwanja vya MTC kutafanyika mchezo wa Shabaha.

Baraza la Michezo ya Majeshi Tanzania (BAMMATA) ni chombo cha kitaalamu cha michezo kilichosajiliwa kwa lengo la kusimamia na kuratibu shughuli za michezo kwa Vyombo vya Ulinzi na Usalama pamoja na Idara Maalum za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ).

BAMMATA lilianzishwa rasmi mwaka 1977 na linajumuisha Kanda nane ambazo ni Kanda ya Ngome, Kanda ya Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), Kanda ya Polisi, Kanda ya Magereza, Kanda ya Uhamiaji, Kanda ya Zimamoto na Uokoaji, Kanda ya Visiwani na Kanda ya SMZ.


NA DENIS MLOWE, IRINGA

MENEJA wa Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) Wilaya ya Iringa, Mhandisi Sadiki Karume, amesema barabara ni miongoni mwa vipaumbele vikubwa katika maendeleo ya wananchi, hivyo taasisi hiyo inaendelea kuchukua hatua kuhakikisha changamoto za miundombinu hiyo zinapatiwa ufumbuzi.

Akizungumza mbele ya Mbunge wa Jimbo la Iringa Mjini, Fadhili Ngajilo, pamoja na wananchi, wa kata ya Makorongoni Mhandisi Karume amesema TARURA inatambua umuhimu wa barabara katika kufungua fursa za kiuchumi, kurahisisha usafirishaji wa bidhaa na kuwawezesha wananchi kufika katika huduma mbalimbali za kijamii.

Amesema miongoni mwa changamoto kubwa zilizowasilishwa ni pamoja na hali ya Kivuko cha Kilongo, ambacho wananchi wamekuwa wakikitaja kutokana na umuhimu wake katika usafiri na shughuli zao za kila siku.

Mhandisi Karume, alisema TARURA iko tayari kushirikiana na Mbunge Ngajilo pamoja na wananchi kuhakikisha changamoto hiyo inafanyiwa kazi kwa kuzingatia umuhimu wake kwa wananchi katika mawasiliano ya barabara
Akizungumza wakati akijibu moja ya maswali ya wananchi waliouliza kuhusu ubovu wa vivuko kwenye korongo la Kilongo amesema timu yake itafika eneo hilo kufanya tathmini ya hali halisi na kuangalia hatua zinazoweza kuchukuliwa ili kupata suluhisho la kudumu.

“Hili tunalichukua kwa uzito wake. Timu yangu tutaweza kufika na kuona tatizo kubwa hili la Kilongo na kuona itatuwaje vipi changamoto ya Kilongo,” amesema Mhandisi Karume.

Aidha, Mhandisi Karume amesema eneo hilo lina vivuko kadhaa vinavyohitaji kuangaliwa, akieleza kuwa TARURA itaendelea kufanya tathmini ya mahitaji ya wananchi na kupanga hatua kulingana na vipaumbele na uwezo wa kifedha.

Kuhusu barabara nyingine zilizotajwa na wananchi kuwa zimeharibika na kuhitaji matengenezo, amesema TARURA imepokea malalamiko na mapendekezo hayo na kwamba baadhi ya barabara tayari zinafanyiwa kazi huku nyingine zikiendelea kufanyiwa tathmini.

Ametaja pia barabara ya Nyingi pamoja na barabara nyingine zilizotajwa katika mikutano ya wananchi, akisema TARURA itaendelea kuzifanyia kazi kulingana na mpango na upatikanaji wa fedha.

Mhandisi Karume amesema pale ambapo matengenezo yanahitaji fedha nyingi zaidi, TARURA inaweza kuwasilisha maombi rasmi kwa ajili ya kutafuta fedha za utekelezaji wa miradi hiyo.

Amesema kuhusu barabara zinazopendekezwa kujengwa kwa kiwango cha lami, TARURA itaendelea kuzipokea na kuzifanyia kazi kwa kuzingatia vigezo vinavyotakiwa, huku akisisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya Serikali, viongozi na wananchi.

Katika hatua nyingine, Mhandisi Karume amesisitiza umuhimu wa kuboresha mawasiliano kati ya TARURA na wananchi kabla na wakati wa utekelezaji wa miradi.

Amesema TARURA itaendelea kutoa taarifa kwa wananchi kabla ya kuanza kwa kazi na wakati kazi zikiendelea ili wananchi waweze kutoa maoni yao na Serikali kupata mrejesho kuhusu utekelezaji wa miradi.

Amesema ushirikiano huo utasaidia kuboresha utekelezaji wa miradi na kuhakikisha changamoto zinazojitokeza zinapatiwa ufumbuzi kwa wakati.

Mbunge wa Iringa Mjini, Fadhili Ngajilo, amekuwa akifanya ziara katika kata mbalimbali za jimbo hilo kwa ajili ya kusikiliza kero za wananchi, ambapo suala la barabara, vivuko na miundombinu mingine limekuwa miongoni mwa changamoto zinazowasilishwa kwake na kupatiwa majibu papo hapo na wataalamu na mengine kuyachukua kupeleka kwenye ngazi za juu.




Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar, Ndugu Abdi Mahamoud Abdi, amesema ameridhishwa na uimara wa Chama Cha Mapinduzi katika Jimbo la Donge, akisema hali hiyo inaonesha umoja na mshikamano uliopo miongoni mwa viongozi na wanachama wa chama hicho.

Ndugu Abdi ameyasema hayo mara baada ya kuwasili katika Tawi la CCM Njia ya Mtoni, Jimbo la Donge, ambako aliweka jiwe la msingi la ujenzi wa tawi hilo, ikiwa ni sehemu ya ziara zake za kukagua na kuimarisha uhai wa Chama Cha Mapinduzi katika matawi mbalimbali.

Amesema umoja na mshikamano unaoonekana katika Jimbo la Donge ni mfano unaopaswa kuigwa na majimbo mengine, huku akisisitiza kuwa mshikamano miongoni mwa viongozi na wanachama ni msingi muhimu katika kukiimarisha na kukiendeleza chama.

Kwa upande wake, Katibu wa Uchumi na Fedha kutoka Afisi Kuu ya CCM Zanzibar, Ndugu Afadhali Taibu Afadhali, amewapongeza wanachama wa CCM Jimbo la Donge kwa kukipa ushindi chama hicho katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025.

Ndugu Afadhali amewataka viongozi na wanachama wa CCM kuendelea kuhamasishana kuhusu ulipaji wa ada za uanachama, akisema hatua hiyo ni miongoni mwa mambo muhimu yanayokiwezesha chama kujiendesha na kuendelea kuwa imara.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa vikao vya matawi kufanyika mara kwa mara ili kujadili changamoto zinazowakabili wanachama, kuzitafutia ufumbuzi na kuhakikisha utekelezaji wa maamuzi unafanyika kwa wakati.

Katika kuendeleza utamaduni wa kujenga mshikamano na kujali viongozi na wanachama, Ndugu Abdi pia aliwatembelea na kuwajulia hali wazee wa chama, akiwemo Katibu Mstaafu wa UWT Tawi la Mto wa Pwani, Ndugu Tatu Hamdani Muhidini, nyumbani kwake Mtambile.

Pia alimtembelea Katibu wa Baraza la Wazee Jimbo la Mahonda, Ndugu Salma Kassim Iddi, ikiwa ni sehemu ya ziara hiyo yenye lengo la kuimarisha mshikamano, upendo na kujali hali za viongozi na wanachama wa Chama Cha Mapinduzi.












Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Deogratius Ndejembi, amefanya ziara ya kushtukiza katika eneo la Mto Ng’ombe, Tandale jijini Dar es Salaam, kukagua hali ya usafi wa mazingira na maandalizi ya kukabiliana na athari zinazoweza kujitokeza katika kipindi cha mvua.

Akiwa ameambatana na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Waziri wa TAMISEMI pamoja na viongozi wa Wilaya ya Kinondoni, Mhe. Ndejembi ameelekeza Mkoa wa Dar es Salaam kuhakikisha mto huo unasafishwa na taka zilizorundikana kandokando ya Mto Ng’ombe zinaondolewa haraka na mazingira yanaendelea kuwekwa katika hali ya usafi.

Amewaagiza Viongozi wa Halmshauri, kupitia maafisa mazingira na maafisa maendeleo, kuendelea kutoa elimu kwa wananchi namna ya kuzingatia usafi na ukusanyaji wa taka. Amesema ni muhimu kwa Halmashauri kuweka miundombinu mizuri ya kukusanya taka na kuzichukua kwa wakati ili wananchi wasitupe taka hizo katika maeneo yasiyofaa.

Vilevile, ameelekeza mamlaka za Wilaya ya Kinondoni kuweka utaratibu wa maeneo rasmi ya kutupa taka ili wananchi wawe na sehemu zinazotambulika kwa ajili ya kuhifadhi taka, hatua itakayosaidia kudhibiti utupaji holela na uchafuzi wa mazingira.

Akizungumza na wananchi wanaoishi pembezoni mwa Mto Ng’ombe, Makamu wa Rais amewataka kuzingatia usafi wa mazingira na kubadili tabia ya utupaji taka holela, akisisitiza kuwa utunzaji wa mazingira unahitaji ushiriki wa Serikali na wananchi kwa pamoja.

Aidha, Makamu wa Rais ameelekeza madaraja yanayokatiza maeneo ya Pakacha na Sokoni katika Mto Kiboko yanapitika wakati wa mvua, ili wananchi waendelee kufanya shughuli zao za kijamii na kiuchumi bila kukwamishwa na changamoto za miundombinu.

















Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba leo (Jumamosi, Septemba 19, 2026) ameshiriki Ibada Kuu na Kufunga Mkutano wa Makambi ya Kanisa la Waadventista Sabato, yaliyofanyika kwa siku saba, Kinyerezi jijini Dar es Salaam

Akizungumza na waumini wa kanisa hilo Dkt. Mwigulu amewasihi waumini wa kanisa hilo kuendelea kudumisha amani na kusimamia maadili ya watoto huku akisisitiza kuwa Serikali itaendelea kulinda uhuru wa wananchi kuabudu kwa kadri ya imani zao.







Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Tanzania inatarajiwa kuwa mwenyeji wa Kongamano la Sita la Jumuiya ya Taasisi za Mitaala Afrika (African Curriculum Association – ACA), litakalofanyika kuanzia Septemba 22 hadi 25, 2026 katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere (JNICC), Dar es Salaam.

Mgeni rasmi katika kongamano hilo la siku nne anatarajiwa kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Deogratias John Ndejembi, ambaye anatarajiwa kuambatana na viongozi mbalimbali wa kitaifa pamoja na wawakilishi wa mashirika ya ndani na nje ya nchi.

Akizungumza na waandishi wa habari kuhusu maandalizi ya kongamano hilo, Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Elimu Tanzania (TET), Dkt. Aneth Komba, amesema TET kwa kushirikiana na Taasisi ya Elimu Zanzibar (TEZ), imepewa nafasi ya kuwa mwenyeji wa kongamano hilo litakalowakutanisha wataalamu na taasisi zinazohusika na ubunifu, uandaaji na uboreshaji wa mitaala barani Afrika.

Amesema kongamano hilo litatoa fursa kwa washiriki kubadilishana maarifa, matokeo ya tafiti, uzoefu na ubunifu kuhusu mabadiliko ya mitaala na mifumo ya elimu, kwa kuzingatia mahitaji ya sasa na ya baadaye ya Afrika na dunia kwa ujumla.

Dkt. Komba amesema Kongamano la ACA 2026 pia litatoa fursa kwa nchi nyingine kujifunza kutoka Tanzania na kushirikishana uzoefu kuhusu mageuzi ya mitaala yaliyofanyika nchini na kuanza kutekelezwa kuanzia Januari 2024.

“Kongamano hili linaendana na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Ajenda 2063 ya Umoja wa Afrika na Lengo la Nne la Maendeleo Endelevu (SDG 4), ambazo zinasisitiza umuhimu wa kutoa elimu bora inayolenga kujenga wahitimu wenye ujuzi na uwezo wa kutumia ujuzi wao kutatua changamoto katika jamii zao,” amesema Dkt. Komba.

Amesema Tanzania imekuwa ikishiriki katika makongamano ya ACA yaliyofanyika katika nchi mbalimbali za Afrika, hivyo kuwa mwenyeji wa kongamano la mwaka huu ni fursa muhimu kwa nchi kuonesha mafanikio yaliyopatikana katika sekta ya elimu.

Kwa mujibu wa Dkt. Komba, mafanikio hayo ni pamoja na maboresho ya Sera ya Elimu na Mafunzo ya Mwaka 2014 Toleo la Mwaka 2023, pamoja na maboresho ya mifumo ya elimu na mitaala.

Amesema kongamano hilo pia litaiwezesha Tanzania kubadilishana uzoefu na kujifunza kutoka nchi nyingine, huku ikichangia katika mwelekeo na maendeleo ya elimu barani Afrika.

Washiriki wa kongamano hilo wanatarajiwa kuwa waandaaji na waendelezaji wa mitaala, watafiti wa elimu, wataalamu na wadau wa mitaala na elimu kwa ujumla kutoka sekta ya umma na binafsi, watunga sera, washirika wa maendeleo na watekelezaji wa mitaala, wakiwemo walimu, wakufunzi, wahadhiri pamoja na wanafunzi wa shahada za uzamili na uzamivu katika masuala ya elimu kutoka Tanzania, Afrika na maeneo mengine duniani.




Bodi ya Maji Bonde la Wami/Ruvu imekutanisha Kikosi Kazi cha Mkoa wa Dar es Salaam na wadau wasafisha mito jijini Dar es Salaam kujadili changamoto zinazoathiri usafi wa vyanzo vya maji na kuweka mikakati ya pamoja ya kukabiliana na athari zinazoweza kujitokeza kutokana na mvua za El Nino zinazotarajiwa kuanza mwezi Oktoba mwaka huu.

Mkurugenzi wa Bodi hiyo, Mhandisi Elibariki Mmassy akizungumza jijini Dar es Salaam, amesema usafi wa mito ni nguzo muhimu katika kulinda vyanzo vya maji, hivyo ushirikiano wa serikali, sekta binafsi na wananchi unahitajika ili kuzuia kuziba kwa njia za maji, mafuriko na uharibifu wa mazingira wakati wa msimu wa mvua.

Kwa upande wake, Katibu Tawala Msaidizi anayesimamia Miundombinu Mkoa wa Dar es Salaam, Mhandisi Amani Mafuru, amesisitiza taasisi na wadau wote kutekeleza wajibu wao kwa wakati ili kuhakikisha mifereji na mito inaendelea kuwa safi, hatua itakayosaidia kupunguza athari zinazoweza kusababishwa na mvua kubwa.

Naye Katibu wa CHAWAMADA, Athumani Kambi, amesema wadau wa usafi wa mazingira wako tayari kushirikiana na mamlaka husika katika kuimarisha shughuli za usafi wa mito, huku akieleza kuwa elimu kwa jamii ni muhimu ili kuondoa tabia ya kutupa taka kwenye vyanzo vya maji.

Mkandarasi Shani Ngwanda amesema utekelezaji wa kazi za usafishaji wa mito utaendelea kuzingatia viwango vya kitaalamu, huku akibainisha kuwa ushirikiano wa wadau wote utasaidia kuongeza ufanisi wa hatua zinazochukuliwa kuimarisha usalama wa mazingira na miundombinu wakati wa msimu wa mvua za El Nino.











Na Mwandishi wetu, Nzega

MWENGE wa uhuru unatarajiwa kuzindua, kukagua, kutembelea na kuweka jiwe la msingi, kwenye miradi ya thamani ya shilingi bilioni 4.1 Wilayani Nzega Mkoani Tabora.

Mkuu wa Wilaya ya Nzega Naitapwaki Tukai ameeleza hayo wakati akikabidhiwa mwenge wa uhuru na Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Uyui Pendo Wella ambaye ni Mkuu wa Wilaya ya Tabora.

DC Tukai amesema ukiwa Wilayani Nzega, mwenge wa uhuru utakimbizwa umbali wa kilometa 223 na kupitia miradi ya thamani ya shilingi bilioni 4.1 ambapo Nzega DC thamani yake ni shilingi bilioni 1.2 na Nzega mji shilingi bilioni 2.9.

Amewapongeza na kuwashukuru wananchi wa maeneo ambayo yamepitiwa na mwenge kwani wamekuwa na hamasa kubwa na mwamko pindi ukipita na kujitokeza kwa wingi kwenye mkesha kata ya Nata.

"Tangu niteuliwe na Mheshimiwa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kuwa DC Nzega miaka minne iliyopita sijawahi kuwaona pamoja wabunge wa majimbo ya Nzega vijijini na Bukene wakiwa pamoja ila leo nimewaona na nimefurahi mno," amesema DC Tukai.

Kiongozi wa mbio za mwenge wa uhuru kitaifa mwaka 2026 Wazo Michael Mwangonda amempongeza DC wa Nzega Naitapwaki Tukai kwa namna alivyosimamia maendeleo ya eneo hilo.

"Leo tumeingia Nzega DC kutoka Uyui na tangu tulivyoanza mradi wa kwanza hadi wa mwisho yote ni mizuri na kesho Nzega mji nasikia mambo ni mazuri huko hongera sana Mkuu wetu wa Wilaya," amesema Mwangonda.

Amewaasa wana Nzega waendelee kumpa ushirikiano wa kutosha mkuu wao wa Wilaya ambaye anamwakilisha Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kwenye eneo hilo.

Mkimbiza mwenge wa uhuru kitaifa mwaka 2026 kutoka mkoa wa Manyara, Inyasi Amsi amempongeza DC Naitapwaki Tukai kwa namna anavyosimamia maendeleo na ushirikiano kwa wana Nzega.

"Hakika Mheshimiwa DC unatuheshimisha wana Manyara kwani watu wa hapa Nzega wanakupenda kutokana na namna unavyowaongoza na kuwasimamia," amesema Inyasi.


Na Janeth Raphael -MichuziTv

Bodi ya Wataalamu wa Ununuzi na Ugavi (PSPTB) imetangaza matokeo ya Mitihani ya Kati Awamu ya Pili ya Taaluma ya Ununuzi na Ugavi iliyofanyika nchini kuanzia Agosti 30 hadi Septemba 4, 2026, huku watahiniwa 275 kati ya 528 waliofanya mitihani hiyo wakifaulu.

Akizungumza leo, Septemba 18, 2026, jijini Dodoma katika mkutano na waandishi wa habari, Mkurugenzi Mtendaji wa PSPTB, Godfred Mbanyi, amesema mitihani hiyo imeendeshwa kwa mujibu wa Sheria ya Bunge Na. 23 ya mwaka 2007 iliyoanzisha Bodi hiyo, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa majukumu yake ya kuendesha mafunzo na mitihani ya kitaaluma katika fani ya Ununuzi na Ugavi.

Amesema jumla ya watahiniwa 567 walidahiliwa kufanya mitihani hiyo, ambapo watahiniwa 528 sawa na asilimia 93.1 walifanya mitihani, huku 39 wakikosa kwa sababu mbalimbali.

Mbanyi amesema kati ya watahiniwa 528 waliofanya mitihani, 275 sawa na asilimia 52.1 wamefaulu, watahiniwa 232 sawa na asilimia 43.9 wamepewa nafasi ya kurudia masomo yao, huku 21 sawa na asilimia 4.1 wakifeli na kutakiwa kuanza upya masomo katika ngazi husika.

Mbanyi ametoa pongezi kwa watahiniwa waliofaulu katika ngazi mbalimbali, wakiwemo waliokidhi vigezo vya kutunukiwa vyeti vya Professional Diploma, Graduate Professional na CPSP, huku akiwapongeza pia wahadhiri na wakufunzi kutoka vyuo na vituo vya mafunzo kwa mchango wao katika kuwaandaa watahiniwa.

Aidha, amesema PSPTB inawaalika watahiniwa waliokamilisha sifa za Professional Diploma I na II, Graduate Professional I, II na III pamoja na Research kushiriki katika Mahafali ya 15 ya Bodi yatakayofanyika kwa ajili ya kutunuku sifa hizo.

Katika hatua nyingine, Mbanyi amewataka watahiniwa ambao hawakufaulu kujisajili na kurudia masomo yao katika Mitihani ya Kati itakayofanyika kuanzia Novemba 9 hadi 13, 2026. Amesema dirisha la usajili limefunguliwa tangu Septemba 8 na litafungwa Oktoba 24, 2026, huku watahiniwa wenye referral status ya nafasi ya mwisho wakitakiwa kutumia mitihani ya Novemba vizuri, kwani baada ya muda huo hadhi hiyo itaondolewa kwa mujibu wa mtaala wa Bodi.

PSPTB pia imewahimiza wanafunzi waliomaliza vyuo vikuu ndani na nje ya Tanzania kujisajili kwa ajili ya mitihani ya kitaaluma ya Bodi ili kupata sifa stahiki katika fani ya Ununuzi na Ugavi. Wazazi, wadhamini na waajiri nao wametakiwa kuwaunga mkono watahiniwa kwa kugharamia ada za maandalizi na mitihani, hatua ambayo itasaidia kuongeza idadi ya wataalamu wenye maarifa na ujuzi katika sekta hiyo muhimu.



Wilaya ya Ngorongoro ipo katika hatua za mwisho ya mapitio na kupitisha mkakati mpya wa miaka mitano unaodhamiria kufanya mageuzi makubwa ya kiuchumi, kijamii na kasi ya maendeleo unaokwenda sambamba dira ya taifa ya maendeleo 2025-2050.

Akifungua kikao maalum cha kupitia mkakati huo  mkuu wa wilaya ya Ngorongoro Brigedia Jenerali Wilson  Sakulo amewataka madiwani wa halmashauri hiyo kutumia fursa hiyo kwa kupanga vipaumbele vitakavyogusa maisha ya wananchi.

“Leo tumekutana hapa kupanga mipango yetu  kwa miaka mitano, hakikisheni mnapanga  vipaumbele vinavyopimika kwa kuangalia maslahi ya wananchi wa wilaya hii ili waweze kupata huduma bora za kijamii, miundombinu na kuboresha shughuli zao za kiuchumi”,alisema Brigedia Jenerali Sakulo.

Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Ngorongoro Mhe. Manja Sironga Yaile aliipongeza Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro kwa kuendelea kuwa mdau muhimu wa maendeleo kutokana na kushiriki kikamilifu katika kuchangia mipango mbalimbali ya kijamii ya Tarafa ya Ngorongoro na wilaya hiyo.

Wakichangia kuhusu mpango mkakati huo baadhi ya madiwani walisisitiza umuhimu wa kujikita katika ujenzi wa barabara,malisho, maji na uimarishwaji wa huduma za kijamii.













Top News