Meneja wa EWURA Kanda ya Magaharibi, Mha. Karim Ally(kushoto) akitoa maelezo ya majukumu yanayotekelezwa na Mamlaka kwa Mkuu wa Wilaya ya Kigoma, Mh. Dkt. Rashid Chuachua(kulia) ikiwemo utoaji wa leseni na vibali vya ujenzi wa vituo vya mafuta, vituo vya CNG, utatuzi wa migogoro na malalamiko na nafasi ya EWURA katika kuweka mazingira wezeshi ya kupata wasambazaji wakubwa wa gesi ya mitungi ( LPG) katika eneo la Kanda ya Magharibi linalohudumia mikoa ya Tabora, Shinyanga, Katavi na Kigoma, wakati kuongozi huyo alipotembelea banda la EWURA katika maonesho ya NaneNane yanayoendelea viwanja vya Ipuli, Tabora, leo 02/08/2026.

Na.Mwandishi Wetu-Tabora

Wakuu wa Wilaya za Tabora, Mh. Upendo Wella, na Kigoma, Mh. Dkt. Rashid Chuachua, wameipongeza EWURA kwa usimamizi mzuri wa huduma za nishati na maji nchini. Wametoa pongezi hizo walipotembelea banda la EWURA, katika maonesho ya NaneNane yanayoendelea viwanja vya Ipuli, Tabora, leo, 02.08.2026.

Viongozi hao wameitaka EWURA kuongeza hamasa kwa wananchi ili kubadili mtazamo na kuhamia katika matumizi ya nishati safi ya kupikia ili azma ya kufikia 80% ya watumiaji ifikapo 2034 itimie.

Aidha, wameisisitiza EWURA kuendelea kuhamasisha uwekezaji wa vituo vya mafuta maeneo ya vijijini, wakieleza kuwa huduma hiyo inahitajika kutokana na kushamiri shughuli za kilimo, ufugaji na uvuvi.

Meneja wa EWURA Kanda ya Magharibi, Mha. Karim Ally, alitumia fursa hiyo kueleza nafasi ya EWURA ya kuweka mazingira wezeshi ya kupata wasambazaji wakubwa wa gesi ya mitungi (LPG) katika eneo la Kanda ya Magharibi linalohudumia mikoa ya Tabora, Shinyanga, Katavi na Kigoma, ambapo kwa sasa ni 19 pekee.

Meneja wa EWURA Kanda ya Magaharibi, Mha. Karim Ally(kushoto) akitoa maelezo ya majukumu yanayotekelezwa na Mamlaka kwa Mkuu wa Wilaya ya Kigoma, Mh. Dkt. Rashid Chuachua(kulia) ikiwemo utoaji wa leseni na vibali vya ujenzi wa vituo vya mafuta, vituo vya CNG, utatuzi wa migogoro na malalamiko na nafasi ya EWURA katika kuweka mazingira wezeshi ya kupata wasambazaji wakubwa wa gesi ya mitungi ( LPG) katika eneo la Kanda ya Magharibi linalohudumia mikoa ya Tabora, Shinyanga, Katavi na Kigoma, wakati kuongozi huyo alipotembelea banda la EWURA katika maonesho ya NaneNane yanayoendelea viwanja vya Ipuli, Tabora, leo 02/08/2026.

Meneja wa EWURA Kanda ya Magahribi, Mha. Karim Ally(kulia) akimweleza Mkuu wa Wilaya ya Tabora, Mh. Upendo Wella (kushoto), Mamlaka inavyoendelea kutoa elimu na kuhamasisha ujenzi wa vituo maeneo ya vijijini ambapo uhitaji bado ni mkubwa hususan katika maeneo ya pembezoni na hivyo kuendelea kuwepo uuzaji holela wa bidhaa za petroli, ambao ni hatari kwa afya, mazingira na maisha ya watu, wakati kiongozi huyo alipotembelea banda la EWURA, katika maonesho ya NaneNane, viwanja vya Ipuli, Tabora, leo, 02/08/2026.




Mkurugenzi wa Idara ya Sera na Mipango wa Wizara ya Viwanda na Biashara, Needpeace Wambuya, amepongeza kasi ya utekelezaji wa majukumu ya Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB), hususan hatua ya kuanzisha mpango wa kuuza mifugo kupitia Mfumo wa Stakabadhi za Ghala.

Akizungumza alipotembelea banda la WRRB katika Maonesho ya Nanenane yanayoendelea viwanja vya John Malecela jijini Dodoma leo Agosti 2, 2026, Wambuya amesema "Niwapongeze sana, kwa kazi nzuri mnayofanya, nimeona mpango wenu kuingiza mifugo kwenye Mfumo wa Stakabadhi za Ghala, natumai mpo hatua nzuri kwasasa."

Kwa upande wake, Ofisa Leseni wa WRRB, Nasri Khea, amesema maandalizi ya mnada wa kwanza wa mifugo kupitia Mfumo huu yamefikia hatua za mwisho, huku mnada huo ukitarajiwa kufanyika hivi karibuni katika Wilaya ya Mvomero.

Amesema pia mfumo huo unakwenda kuingiza kuwezesha biashara za bidhaa mbalimbali ikiwamo Mwani na mahindi.
*Wananchi wakumbushwa kuchukua Amana zao zilizokuwa Benki ya FBME

Na Mwandishi Wetu, Dodoma
BODI ya Bima ya Amana (DIB) imewataka wananchi kutembelea Maonesho ya Kimataifa ya Wakulima ya Nane Nane ili kupata elimu kuhusu ulinzi wa amana zao na taratibu za kufidiwa fedha wanazoweka katika benki na taasisi za fedha zilizopewa leseni na Benki Kuu ya Tanzania (BoT).

Akizungumza katika maonesho hayo yanayoendelea katika Viwanja vya Dkt. John Samwel Malecela jijini Dodoma, Mkurugenzi Mkuu wa DIB, Isack Kihwili, amesema wananchi wanapaswa kuhakikisha wanaweka fedha zao katika benki na taasisi za fedha zilizosajiliwa na kupewa leseni na Benki Kuu ya Tanzania.

Amesema kufanya hivyo ni muhimu kwa kuwa kuweka fedha katika taasisi zisizo rasmi kunaweza kuwanyima wananchi haki ya kupata fidia endapo taasisi hizo zitashindwa kutekeleza majukumu yake au kushindwa kurejesha fedha za wenye amana.

Kihwili pia amewataka wenye amana katika iliyokuwa Benki ya FBME ambao bado hawajachukua fedha zao kujitokeza haraka ili kukamilisha mchakato wa malipo, akisema fedha zao bado zinawasubiri.

Amesema DIB imefikia hatua kubwa katika kulipa madai ya wenye amana wa benki hiyo, huku akibainisha kuwa ni asilimia ndogo tu ya walengwa ambao bado hawajajitokeza kuchukua fedha zao.

Kwa mujibu wa Kihwili, madai ya wenye amana wa FBME kwa upande wa Tanzania yalifikia takribani Sh bilioni 35, ambapo hadi sasa zaidi ya asilimia 85 ya fedha hizo tayari zimelipwa kwa walengwa.

Amesema bado kuna takribani watu 428 ambao hawajajitokeza kuchukua fedha zao zenye thamani ya karibu Sh bilioni nne, licha ya fedha hizo kuwa tayari zimetengwa kwa ajili yao.

“Tunawasihi wale ambao bado hawajajitokeza kuchukua fedha zao wafanye hivyo haraka, kwa sababu fedha hizo zimetengwa na zipo tayari kwa ajili ya malipo,” amesema.

Amefafanua kuwa baada ya kundi hilo kujitokeza na kulipwa fedha zilizotengwa kwa ajili yao, hatua inayofuata itakuwa ni kulipa asilimia 15 iliyobaki ili kuhakikisha kila mwenye amana anayestahili fidia analipwa madai yake kwa asilimia 100, kwa kuzingatia taratibu zinazotumika.


Aidha, Kihwili amesema bado kuna kundi la wadai wengine, wakiwemo baadhi ya wafanyakazi waliokuwa na madai yaliyofikishwa mahakamani, ambao malipo yao hayajahusishwa katika awamu inayoendelea kutokana na mchakato wa kufuatilia na kuhakiki mali za benki hiyo.

Amesema DIB inaendelea kufuatilia mali zilizobaki za benki hiyo ili kuhakikisha fedha za kutosha zinapatikana na kuwezesha kukamilishwa kwa malipo ya wadai hao kwa kuzingatia taratibu za kisheria.

Na Mwandishi Wetu, Dodoma
MAMLAKA ya Udhibiti wa Mbolea Tanzania (TFRA) imesema Maonesho ya Kilimo na Mifugo ya Nane Nane ni fursa muhimu kwa wakulima kupata elimu na taarifa zitakazowasaidia kujiandaa kwa msimu wa kilimo wa mwaka 2026/2027.

Akizungumza katika Maonesho ya Kilimo na Mifugo ya Nane Nane yanayoendelea katika Viwanja vya Dkt. John Malecela jijini Dodoma, Mkurugenzi wa Huduma za Udhibiti Ubora wa TFRA, Happiness Mbelle, amesema wakulima wanapaswa kuhakikisha taarifa zao zimesajiliwa na kuhuishwa kwa wakati ili kuepuka changamoto wakati wa usambazaji wa mbolea.

Amesema mbolea inapatikana kwa kiasi cha kutosha, huku akiwataka wakulima kushirikiana na maafisa ugani katika kupima udongo ili kubaini mahitaji sahihi ya mbolea kulingana na aina ya mazao na hali ya udongo.

“Mkulima anapaswa kushirikiana na maafisa ugani kupima udongo ili kubaini mahitaji ya mbolea. Hii itasaidia kutumia mbolea kwa usahihi na kuongeza tija katika uzalishaji,” amesema Mbelle.

Aidha, amesema maonesho hayo ni fursa kwa wananchi kutoka maeneo mbalimbali nchini kupata elimu kuhusu matumizi sahihi ya mbolea, pamoja na huduma na majukumu ya TFRA.

Amesema TFRA itaendelea kutoa elimu kwa wananchi katika maeneo mbalimbali nchini ili kuwawezesha kuelewa majukumu ya mamlaka hiyo na kuhakikisha wanapata huduma bora zenye viwango.

Mbelle amewataka wakulima kutumia fursa ya maonesho hayo kupata elimu na ushauri kutoka kwa wataalamu ili kuongeza ufanisi na tija katika shughuli za kilimo.

Na Mwandishi Wetu, Dodoma
BARAZA la Taifa la Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (NACTVET) limesema Maonesho ya Kilimo na Mifugo ya Nane Nane ni fursa muhimu ya kutoa elimu kwa wanafunzi na wahitimu wa vyuo vya kati vinavyotoa mafunzo katika fani za kilimo na mifugo kuhusu fursa za kujiajiri katika sekta hizo.

Akizungumza katika Maonesho ya Kilimo na Mifugo ya Nane Nane yanayoendelea katika Viwanja vya Dkt. John Malecela, jijini Dodoma, Afisa Udhibiti Ubora wa NACTVET, Doris Chiwambo, amesema sekta ya kilimo ina fursa kubwa za ajira na kujiajiri, hivyo wahitimu wa fani za kilimo na mifugo wanapaswa kutumia ujuzi walioupata kuanzisha shughuli za uzalishaji.

Amesema wahitimu hao wanaweza kujiajiri kupitia shughuli mbalimbali ikiwemo kilimo, ufugaji na utoaji wa elimu na huduma za kitaalamu katika sekta hizo.

“Sekta ya kilimo ina fursa nyingi za ajira na kujiajiri. Wahitimu wa fani za kilimo na mifugo wanaweza kutumia elimu na ujuzi walioupata kujiajiri katika kilimo, ufugaji na hata kutoa elimu kwa jamii,” amesema Chiwambo.

Aidha, amesema maonesho hayo ni fursa pia kwa wananchi wanaopanga kuanzisha vyuo vinavyotoa mafunzo ya kilimo, mifugo na uvuvi kupata elimu na maelekezo kuhusu taratibu na vigezo vya kuanzisha na kuendesha vyuo hivyo.

Chiwambo amesema NACTVET itaendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu majukumu yake, pamoja na kuhakikisha jamii inaelewa huduma zinazotolewa na baraza hilo ili kufanikisha lengo la kutoa elimu na mafunzo yenye viwango vinavyokidhi mahitaji ya soko la ajira.

Ameongeza kuwa ushiriki wa NACTVET katika maonesho hayo unalenga kuongeza uelewa kwa wananchi kuhusu umuhimu wa elimu na mafunzo ya ufundi stadi, pamoja na fursa zinazopatikana kupitia taaluma za kilimo, mifugo na uvuvi.

 

MKUU wa Kampasi ya Dodoma wa Chuo cha Uhasibu Arusha,Prof. Epaphra Manamba,akizungumza na waandishi wa habari leo Agosti 2,2026 kwenye banda la chuo hicho akimwakilisha Mkuu wa Chuo, Profesa Eliamani Sedoyeka,wakati wa Maonesho ya 49 ya Kilimo ya Nane Nane yanayoendelea katika viwanja vya Dkt. John Samuel Malecela Nzuguni jijini Dodoma kwa niaba ya 

.....

MKUU wa Kampasi ya Dodoma wa Chuo cha Uhasibu Arusha,Prof. Epaphra Manamba,amesema wanaendelea kuandaa wataalamu wenye ujuzi na uwezo wa kutumia teknolojia za kisasa katika uzalishaji, usimamizi na biashara ya mazao, hatua itakayochangia kuongeza tija, ushindani na thamani ya sekta ya kilimo nchini.

Akizungumza katika Maonesho ya 49 ya Kilimo ya Nanenane yanayoendelea katika viwanja vya Dkt.John Malecela Nzunguni jijini Dodoma, Mkuu wa Kampasi ya Dodoma wa Chuo cha Uhasibu Arusha, Prof.Epaphra Manamba, akimwakilisha Mkuu wa Chuo, Profesa Eliamani Sedoyeka, amesema IAA imeamua kushiriki maonesho hayo ili kuwa karibu na wakulima, kutoa elimu na kuonesha mchango wa taaluma katika kuimarisha uzalishaji wa kilimo nchini.

Amesema sekta ya kilimo ndiyo uti wa mgongo wa uchumi wa Tanzania kwa kuwa inategemewa na takribani asilimia 65 ya nguvu kazi ya Taifa, lakini bado mchango wake katika Pato la Taifa ni takribani asilimia 26 pekee, hali inayoonesha kuwa kuna nafasi kubwa ya kuongeza tija kupitia matumizi ya maarifa, teknolojia na usimamizi bora wa biashara.

"Kilimo kinahitaji nguvu kazi yenye ujuzi, ubunifu na maarifa ya kisasa. Ndiyo maana Chuo cha Uhasibu Arusha kinaendelea kutoa programu mbalimbali za biashara, uchumi, fedha na teknolojia ili kuwajengea uwezo wataalamu watakaosaidia kuifanya sekta ya kilimo iwe yenye ushindani na yenye mchango mkubwa zaidi katika uchumi wa Taifa," amesema Prof.Manamba.

Ameeleza kuwa pamoja na changamoto za mitaji zinazowakabili wakulima wengi pamoja na utegemezi wa zana duni za kilimo, bado kuna fursa kubwa ya kuongeza uzalishaji endapo wakulima wataunganishwa na taasisi za kifedha pamoja na huduma za kitaalamu zitakazowezesha upatikanaji wa mitaji na uwekezaji katika teknolojia za kisasa.

Prof.Manamba amesema IAA imejikita pia katika kufundisha teknolojia zinazoibukia ikiwemo Akili Unde (Artificial Intelligence - AI), ambapo wanafunzi wa chuo hicho tayari wamebuni mifumo inayotumia AI kuboresha uzalishaji wa mazao kama vitunguu kwa lengo la kuongeza tija, kupunguza gharama za uzalishaji na kuifanya kilimo kuwa biashara yenye faida zaidi.

"Hatutaki kuona kilimo kinabaki kwa ajili ya kujikimu pekee. Tunataka wakulima walime kwa mtazamo wa biashara, waongeze thamani ya mazao yao na kuongeza kipato cha familia zao pamoja na kuchangia zaidi katika uchumi wa Taifa," amsisitiza.

Akizungumzia kaulimbiu ya Nanenane ya mwaka huu isemayo "Tambua Soko, Ongeza Tija, Tekeleza Dira ya Taifa 2050," Prof.Epaphra Manamba amesema dira hiyo inalenga kujenga nguvu kazi yenye ujuzi na maarifa inayoweza kuleta mapinduzi katika sekta mbalimbali za uchumi, hususan kilimo.

Amebainisha kuwa taasisi za elimu zina jukumu la kuhakikisha zinatoa wahitimu wenye ujuzi unaoendana na mahitaji ya soko la ajira na mabadiliko ya teknolojia ili kuongeza ufanisi katika uzalishaji na kuifanya Tanzania kufikia malengo ya maendeleo ya Dira ya Taifa 2050.

Amesema kupitia ushiriki wa Maonesho ya Nanenane, Chuo cha Uhasibu Arusha kinaendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu programu zake mbalimbali na namna zinavyoweza kuwaandaa vijana kuwa wataalamu watakaochangia maendeleo ya kilimo, biashara na uchumi wa kidijitali nchini.

▪️Awataka watumishi kutimiza wajibu wao

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amewahimiza watendaji wa Serikali kuwahudumia kikamilifu Watanzania ili miradi inayojengwa na Serikali itoe matokeo chanya.

“Tunachokijenga hapa, si jengo pekee, bali tunajenga mazingira bora ya utendaji wa mfuko. Kupitia uwekezaji huu tunachochea na tunaharakisha utekelezaji wa dhamira ya dhati aliyoionesha Mheshimiwa Rais kumsaidia mkulima mdogo kwa kuwezesha kupata mikopo.”

“Watumishi wote wanapaswa kutimiza wajibu wao kwa bidii ili uwekezaji huu uwe na manufaa kwa Taifa. Tusiweke ofisi nzuri halafu huduma zikawa duni, tutakua hatujafikia malengo yaliyokusudiwa, ofisi nzuri lakini mwananchi akija kupata huduma anaambiwa njoo kesho, njoo kesho, majengo haya hayatakuwa na maana,” amesema Waziri Mkuu.

Waziri Mkuu ameyasema hayo leo (Jumapili Agosti 2, 2026) Iyumbu jijini Dodoma wakati akiweka jiwe la msingi la ujenzi wa makao makuu ya ofisi za Mfuko wa Udhamini wa Pembejeo za Kilimo (AGITF).

Dkt. Mwigulu amesisitiza kuwa uwekezaji huo unaofanywa na Serikali katika utafiti wa kilimo ni mwelekeo sahihi wa mageuzi katika sekta ya kilimo. “Kuwekeza kwenye utafiti ni njia sahihi ya kufanya mageuzi katika sekta husika, tumetoka kufanya uzinduzi wa makao makuu ya taasisi yetu ya utafiti wa kilimo, na pembeni yake kuna jengo zuri la maabara ya kilimo, kuonesha jinsi Rais anamaanisha kwa dhati kufanya mageuzi katika kilimo.”

“Kwa nchi nyingine maabara ile ya kisasa ingekuwa kwenye moja ya chuo kikuu, lakini ile ni maabara ya wizara na ipo hapa makao makuu ya nchi,” ameongeza Waziri Mkuu.

Awali akiwa katika mji wa Serikali - Mtumba, kwenye halfa ya uwekaji wa jiwe la msingi la ujenzi wa ofisi za makao makuu ya Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI), Waziri Mkuu alimpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendeleza uwekezaji jijini Dodoma hali iliyochochea ukuaji wa mkoa huo.

Dkt. Mwigulu ameongeza kuwa hatua hiyo ya Rais Samia imeenda sambamba na kuwaamini wakandarasi wazawa jambo lililowakuza wakandarasi hao.

“Mheshimiwa Rais aliweka imani kwao, akasema waacheni wajenge. Tumeona majengo na miradi ikimeremeta….nilipita katika miradi ya sekta nyingine, nikakuta madaraja yenye urefu wa ghorofa yamejengwa na wakandarasi wazawa, zaidi ya madaraja 81, sasa ukiangalia kwa jicho la kibinafsi utasema si ni yule mmoja tu ndiyo akapata mradi, lakini niwaambieni huo ni mzunguko wa uchumi wa ndani ya nchi, ndiyo maana mabenki yanapata wateja na yamepunguza mikopo chechefu,” amesisitiza Waziri Mkuu.

Mapema, akimkaribisha Waziri Mkuu, Waziri wa Kilimo, Daniel Chongolo amemshukuru Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuiwezesha wizara hiyo kupata bajeti ya kutosha kuendesha shughuli zake, ikiwemo kuwaongezea bajeti kila mwaka.














NA DENIS MLOWE - DAR ES SALAAM

VICTORIA Group (VG) imetangaza kuandaa mbio za afya za VG Fun Run zitakazofanyika Agosti 8, 2026 katika viwanja vya Victoria Park, Ununio jijini Dar es Salaam, zikiwa na lengo la kuhamasisha afya, kuimarisha mshikamano wa wanachama na kuwashirikisha wananchi katika mazoezi ya mwili.

Akizungumza na waandishi wa habari, Mwenyekiti wa Kamati ya VG Fun Run, Isidori Msaki, alisema wazo la kuanzisha mbio hizo limetokana na ukweli kuwa Victoria Group imekuwa pamoja kwa zaidi ya miaka 26 na sasa wanachama wengi wamefikisha umri wa zaidi ya miaka 50, jambo lililowasukuma kuweka kipaumbele kwenye afya zao.

Alisema Victoria Group ina wanachama 113 ambao pamoja na familia zao wanafikia takribani watu 700, hivyo wameona ni muhimu kuanzisha shughuli ya pamoja itakayowahamasisha kufanya mazoezi na kuishi maisha yenye afya.

Msaki alisema mbio hizo zitahusisha kukimbia umbali wa kilomita 10 kuanzia saa 12:00 asubuhi, huku washiriki wote watakaomaliza wakitunukiwa medali na kuandaliwa huduma ya supu, wakati wadhamini wa tukio watapatiwa vyeti vya shukrani kwa mchango wao.

Alisema tukio hilo halitawahusu wanachama wa Victoria Group pekee, bali pia limefunguliwa kwa marafiki na wananchi wote wanaotaka kushiriki.

Msaki alisema washiriki kutoka nje ya Victoria Group watatakiwa kulipa shilingi 30,000 ambazo zitajumuisha fulana maalumu, namba ya ushiriki pamoja na medali baada ya kumaliza mbio.

Aliongeza kuwa kwa wale wasioweza kushiriki mbio za kilomita 10, waandaaji wameandaa programu maalumu ya mazoezi ya aerobics itakayofanyika katika Victoria Park chini ya wakufunzi wa mazoezi, sambamba na burudani ya muziki na shughuli nyingine za kijamii.

Msaki alisema hadi sasa zaidi ya washiriki 126 wamekwishajisajili, huku matarajio yakiwa kufikisha zaidi ya washiriki 200 kabla ya siku ya tukio.

Naye Mwenyekiti wa Victoria Group, Sabasaba Mushingi, alisema kikundi hicho kilianzishwa takribani miaka 26 iliyopita kwa lengo la kujenga mshikamano na kusaidiana katika nyakati za furaha na huzuni, lakini kadiri miaka ilivyokwenda wamepanua shughuli zao hadi kwenye uwekezaji wa kiuchumi.

Alisema kwa sasa Victoria Group inamiliki vitega uchumi mbalimbali ikiwemo Victoria Park yenye thamani inayokadiriwa kuzidi shilingi bilioni moja kwa tathmini ya sasa, pamoja na uwekezaji katika hati fungani za Serikali na hisa.
Mushingi alisema VG Fund Run ni mwanzo wa safari ya kulifanya tukio hilo kuwa moja ya mbio kubwa nchini, zitakazokuwa zikifanyika kila mwaka na kuvutia washiriki wengi zaidi kutoka ndani na nje ya Victoria Group.

Alieleza kuwa baada ya tathmini ya tukio la mwaka huu, uongozi unapanga kuliboresha zaidi ili katika miaka ijayo liwe na zawadi kubwa, washiriki wengi zaidi na pia liwe jukwaa la kuchangisha fedha kwa ajili ya kusaidia jamii kupitia miradi mbalimbali ya kijamii.

Aliwahimiza wananchi kujitokeza kwa wingi Agosti 8 katika Victoria Park, Ununio, kushiriki siku ya mazoezi, afya na burudani, akisisitiza kuwa lengo kuu la Victoria Group ni kujenga jamii yenye afya bora huku ikiendeleza mshikamano na utamaduni wa kusaidiana.






Chama Kikuu cha Ushirika Tunduru (TAMCU) kimetangaza kufunguliwa kwa msimu mpya wa ununuzi wa zao la mbaazi utakaoanza katikati ya mwezi Agosti, huku kikieleza kuwa kimejipanga kuhakikisha uzalishaji unaongezeka na wakulima wanalipwa kwa wakati kupitia mfumo wa stakabadhi za ghala.

Akizungumza na waandishi wa habari Agosti 2, 2026, katika Maonesho ya Kilimo Nanenane Kitaifa, Mjumbe wa Bodi ya TAMCU, Nurdin Raisi Chakilo, alisema chama hicho tayari kimefunga msimu wa zao la ufuta na sasa kinaelekeza nguvu katika maandalizi ya msimu wa mbaazi.

Alisema TAMCU imejipanga kuhakikisha mnyororo mzima wa mfumo wa stakabadhi za ghala unafanya kazi kwa ufanisi, huku ikiwahamasisha wakulima kukusanya mazao yao, kuyaandaa kwa ubora na kuyapeleka kwenye maghala ya mnada ili kupata soko na malipo kwa wakati.

Chakilo alisema chama hicho kinajivunia mafanikio ya mfumo huo kutokana na minada kufanyika kwa wakati na wakulima kulipwa kwa wakati, hali iliyoongeza uelewa na imani ya wakulima katika mfumo wa stakabadhi za ghala.

Aidha, alisema TAMCU imeongeza thamani ya mali zake kutoka shilingi bilioni 1.5 hadi kufikia shilingi bilioni 5, sambamba na kuanzisha mradi wa usafirishaji wa mazao na mizigo mchanganyiko unaotoa huduma katika maeneo mbalimbali nchini kwa kutumia magari yenye uwezo wa kubeba tani 32 kwa kila safari.

Aliongeza kuwa chama hicho kimejipanga kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kupitia mpango wa kujenga kiwanda cha korosho wilayani Tunduru pamoja na jengo la utawala lenye ghorofa tano litakalokuwa na ukumbi wa watu zaidi ya 700, ofisi za TAMCU na maeneo ya kupangisha.

Chakilo alisema TAMCU, inayohudumia vyama vya msingi Wilayani Tunduru Mkoani Ruvuma pamoja na baadhi ya wakulima wa mkoa jirani wa Njombe kwa zao la korosho, kimeendelea kunufaika na jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita kupitia upatikanaji wa pembejeo za kilimo, hatua iliyochangia kuongeza tija katika uzalishaji wa mazao.


Kampuni ya mawasiliano ya Yas Tanzania imezindua rasmi mnara wa 5G wilayani Masasi, Mkoa wa Mtwara, hatua inayotarajiwa kuongeza kasi ya biashara, kuboresha upatikanaji wa huduma za kidijitali na kufungua fursa mpya za maendeleo kwa wakazi wa wilaya hiyo na maeneo ya jirani.

Uwekezaji huo ni sehemu ya mkakati wa Yas wa kuendelea kusogeza teknolojia ya kisasa karibu na wananchi ili kuwawezesha kunufaika na uchumi wa kidijitali kupitia mawasiliano yenye kasi, uhakika na ubora.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mkuu wa Yas Kanda ya Pwani Kusini, Bi. Fadhila Saidi, alisema kampuni inaendelea kuwekeza katika miundombinu ya kisasa ya mawasiliano ili kuhakikisha Watanzania wanapata suluhisho zinazowawezesha kuboresha maisha na kukuza shughuli zao za kiuchumi.

"Tunazindua mnara huu wa 5G kwa lengo la kuhakikisha wakazi wa Masasi na mkoa wa Mtwara kwa ujumla wanapata huduma za mawasiliano zenye kasi na ubora ili kuchochea shughuli za kiuchumi na mawasiliano ya uhakika. Kwetu sisi, teknolojia ni nyenzo ya kuwawezesha Watanzania kufikia fursa zaidi za maendeleo," alisema Bi. Saidi.

Aliongeza kuwa, Wilaya ya Masasi ina wakazi zaidi ya 315,000 wanategemea kilimo na biashara, hivyo uzinduzi wa teknolojia ya 5G wilayani humo utachochea shughuli mbalimbali za kimaendeleo, kwani wakulima wataweza kufuatilia bei za mazao na kuwasiliana moja kwa moja na masoko, huku wafanyabiashara wakipanua biashara zao kupitia majukwaa ya kidijitali na mifumo ya kisasa ya malipo”.

Bi. Saidi alisema huduma hiyo pia itawanufaisha vijana kwa kuwafungulia fursa za ajira, ubunifu na ujasiriamali kidijitali, huku wanafunzi na walimu wakipata urahisi wa kutumia majukwaa ya kujifunzia mtandaoni. Aidha, taasisi za afya na huduma nyingine za kijamii zitanufaika na mawasiliano yenye kasi na uhakika yatakayoongeza ufanisi katika utoaji wa huduma.

Aliongeza kuwa, sambamba na uwekezaji katika mawasiliano, kwa upande wa Mixx, Kampuni inaendelea kuwawezesha wananchi kutuma na kupokea fedha, kulipa bili, kufanya malipo ya biashara na kupata huduma mbalimbali za kifedha kwa usalama na urahisi, hatua inayochochea ujumuishaji wa kifedha na ukuaji wa uchumi wa wananchi.

Kwa upande wake, mkazi wa Masasi na mfanyabiashara, Bw. Jaffari Wadi, alisema uzinduzi wa mnara huo wa 5G utakuwa chachu ya kukuza biashara katika eneo hilo.

"Uzinduzi wa mnara huu wa 5G utatusaidia kwa kiasi kikubwa kuchochea ukuaji wa biashara zetu kwani huduma sasa zitakuwa za haraka zaidi. Tutakuwa na uwezo wa kuwasiliana kwa urahisi na wateja, kufanya miamala kwa wakati na kutumia fursa za biashara mtandaoni ambazo hapo awali zilikuwa changamoto kutokana na kasi ya mtandao," alisema Bw. Wadi.

Yas imeendelea kuwekeza katika upanuzi wa mtandao wake nchini ikiwa ni sehemu ya dhamira yake ya kuhakikisha hakuna Mtanzania anayebaki nyuma katika safari ya mageuzi ya kidijitali. Kampuni hiyo inaamini kuwa upatikanaji wa miundombinu ya mawasiliano yenye ubora ni msingi wa kukuza biashara, kuimarisha ujumuishaji wa kidijitali na kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Uzinduzi wa mnara wa 5G Masasi unaongeza hatua nyingine katika juhudi za Yas za kuendelea kuwapatia Watanzania suluhisho za mawasiliano na kifedha zinazowawezesha kufungua fursa mpya za maendeleo na kushiriki kikamilifu katika uchumi wa kidijitali.
Mkuu wa Yas Kanda ya Kusini, Bi. Fadhila Saidi (kulia), akiwa pamoja na Mwenyekiti wa Mtaa wa Majimaji, Wilaya ya Masasi, Bw. Bakari Issa (kushoto), wakikata utepe kuashiria uzinduzi rasmi wa mnara wa 5G wa Yas katika Wilaya ya Masasi, Mkoa wa Mtwara, hivi karibuni. Teknolojia hiyo inatarajiwa kuboresha huduma za intaneti ya kasi, kuchochea ukuaji wa biashara na kuongeza upatikanaji wa huduma za kidijitali kwa wakazi wa Masasi na maeneo ya jirani.


NA: MWANDISHI WETU, PANGANI

Viongozi na watendaji wa matawi wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM), wilaya ya Pangani mkoani Tanga, wamepatiwa mafunzo ya kuwajengea uwezo wa masuala mbalimbali ya kichama, kiuongozi na kijamii ili kuboresha utendajikazi wao wa kila siku.

Mafunzo hayo yametolewa Agosti 2, 2026, katika Kata ya Kipumbwi wilayani humo.

Akizungumza katika mafunzo hayo, Mwenyekiti wa Seneti ya vyuo vya kati, vyuo na vyuo vikuu mkoa wa Tanga, Leila Mnaki, ambaye alikuwa miongozo mwa wakufunzi, amesema CCM ni Chama imara kwani misingi yake ipo ngazi za chini za mabalozi na matawi, hivyo ni wajibu wa Chama kutoa mafunzo ya mara kwa mara kwa viongozi wake ili kuboresha utendajikazi.

"Nguvu ya Chama ni wanachama na viongozi wake, ndiyo maana tupo hapa kupata mafunzo ya kutujengea uwezo ili utendajikazi wetu uwe wenye tija kwa manufaa ya Chama na wananchi tunaowahudumia," amesema Mnaki.

Aidha, Mnaki amesema, ni wajibu wa viongozi kuwahudumia wananchi kwa kufuata misingi ya Chama, ambayo imesisitiza kutanguliza maslahi ya wananchi ili kukuza maendeleo.

"Chama chetu hakiongozwi kwa utashi wa mtu, bali kanuni, miongozo na taratibu, ni matumaini yangu kuwa viongozi na watendaji mtazingatia hili katika Utumishi wenu wote," ameongeza.

Awali, mratibu wa mafunzo hayo, ambaye pia ni Katibu wa UVCCM wilaya, Nasri Mkalipa, aliwasisitiza viongozi hao kuzingatia yote na kuyatendea kazi.

"Niwasihi sana tuzingatie yote tutakayofundishwa hapa, kwani mafunzo haya ni mahsusi katika kuboresha utendajikazi wetu na kuonyesha utofauti wa kiuongozi," amesema Mkalipa.

Katika mafunzo hayo, mada mbalimbali zilifundishwa kwa viongozi hao. Miongoni mwa mada hizo ni pamoja na itikadi, kanuni na falsafa ya CCM, uandishi wa muhtasari na utunzaji kumbukumbu.

Pia, masuala ya uongozi wa kimkakati, ukatili wa kijinsia, afya ya akili, usalama barabarani na matumizi ya mitandao ya kijamii.

Ikumbukwe kuwa, mafunzo hayo maalum yamepewa jina la "Darasa la Ushindi" huku yakichagizwa na kaulimbiu ya "T3 - Tujifunze, Tuongoze na Tuwajibike".

Kimsingi, mkakati uliopo ni kufikisha mafunzo hayo katika kata zote 14 za wilaya hiyo, huku walengwa wa mafunzo hayo wakiwa ni wenyeviti, makatibu na makatibu hamasa wa UVCCM wa matawi yote wilayani humo.







Na Janeth Raphael - MichuziTv.

Serikali imesisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano kati ya sekta za kilimo, mifugo, uvuvi, viwanda, biashara na taasisi za kifedha ili kuongeza uzalishaji, kuimarisha uchakataji wa mazao na kuchochea ukuaji wa uchumi wa Taifa.

Msisitizo huo umetolewa leo Agosti 2, 2026 jijini Dodoma na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar, alipofanya ziara katika Viwanja vya Dk. John Samwel Malecela, Nzuguni, kujionea shughuli mbalimbali zinazoendelea katika Maonesho ya 33 ya Kimataifa ya Kilimo (Nanenane).

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Balozi Omar amesema maendeleo ya uchumi hayawezi kufikiwa kwa ufanisi ikiwa kila sekta itafanya kazi kwa kujitegemea, akieleza kuwa ushirikiano wa karibu kati ya sekta hizo ni msingi wa kuongeza tija, kuvutia uwekezaji na kuinua kipato cha wananchi.

Amesema Serikali inalenga kuona uzalishaji unaongezeka sambamba na kuongeza thamani ya mazao kupitia uchakataji, huku taasisi za kifedha zikiendelea kuwezesha maeneo yenye kipaumbele ili kuharakisha maendeleo ya sekta za uzalishaji.

"Ni muhimu kuwa na mtazamo wa pamoja wa kukuza uzalishaji, kuongeza thamani ya mazao kupitia uchakataji na kuhakikisha sekta zote zinashirikiana kwa manufaa ya wananchi na uchumi wa Taifa. Taasisi za kifedha zinapaswa kuendelea kuunga mkono maeneo ambayo Serikali imeyapa kipaumbele ili kuongeza kasi ya uwekezaji," amesema.

Katika hatua nyingine, Waziri huyo amesema Serikali inaendelea kufuatilia matumizi ya matrekta yaliyotolewa kwa wakulima ili kuhakikisha yanatumika katika maeneo yaliyokusudiwa na kuchangia kuongeza tija katika uzalishaji wa kilimo.

Aidha, amewapongeza wajasiriamali wanaozalisha bidhaa zenye ubora, huku akisisitiza umuhimu wa kuweka mikakati madhubuti ya kutafuta masoko ya ndani na nje ya nchi ili kuongeza ushindani wa bidhaa zinazozalishwa Tanzania.

Ameongeza kuwa pamoja na kuongeza uzalishaji, kuna haja ya kuwekeza zaidi katika utangazaji wa bidhaa, kuimarisha mifumo ya masoko na kuboresha mazingira ya biashara ili bidhaa za Kitanzania zipate nafasi kubwa katika masoko ya kikanda na kimataifa.






Top News