

Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imewataka Waandishi wa Habari wa Crown Media kulinda imani ya umma kwa kuzingatia weledi, maadili, uadilifu na uwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu yao.
Wito huo umetolewa wakati wa mafunzo ya siku mbili yaliyotolewa na JAB kwa Waandishi wa Habari wa Crown Media, kuanzia Agosti 18 hadi 19, 2026, jijini Dar es Salaam yakilenga kuwaongezea maarifa na kuwajengea uwezo wa kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia sheria, maadili na viwango vya taaluma ya uandishi wa habari.
Akiwasilisha Mada kuhusu Msingi na Mfumo wa Kisheria unaosimamia Sekta ya Habari nchini Tanzania katika mafunzo hayo, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa JAB, Wakili Patrick Kipangula, amewasihi Waandishi wa Habari kuthamini na kulinda taaluma yao kwa kuzingatia misingi inayowaongoza katika utekelezaji wa majukumu yao.

Kwa upande wake, Dkt. Egbert Mkoko amewataka Waandishi wa Habari kuzingatia maadili katika kila hatua ya kazi zao, akieleza kuwa maadili ndiyo msingi wa uandishi wa habari unaowajibika na wenye tija kwa jamii.
“Mwandishi wa Habari anapaswa kuzingatia maadili ya kazi katika kila hatua ya utekelezaji wa majukumu yake, kwa kuwa uadilifu na uwajibikaji ndiyo msingi wa taaluma hii,” amesema Dkt. Mkoko alipokuwa akifafanua mada Kuhusu Maadili ya Utangazaji na makosa ya kimaadili yanayofanywa mara kwa mara.
Naye Mjumbe wa JAB na Kaimu Meneja wa Huduma za Kiswahili wa Shirika la Magazeti ya Serikali (TSN), Bw. Mgaya Kingoba, akiwasilisha mada kuhusu uzalendo, amewataka Waandishi wa Habari kutumia taarifa kwa usahihi na kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia maslahi ya umma.

“Kwa kweli, changamoto tuliyonayo katika vyombo vyetu vya habari ni kushindwa kutofautisha maoni binafsi na uchambuzi wa kitaaluma, pamoja na kushindwa kutenganisha nafasi ya mtu binafsi na wajibu wake kama mwanataaluma. Pia kumekuwa na dhana kwamba Bodi ipo kwa ajili ya kuwadhibiti Waandishi wa Habari, pamoja na uelewa mdogo kuhusu ithibati, umuhimu wake na nafasi yake katika kulinda heshima ya taaluma,” amesema Imani Luvanga mmoja wa washiriki.
Mafunzo hayo ni sehemu ya utekelezaji wa majukumu ya JAB kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229, yanayolenga kuimarisha weledi, uadilifu, uwajibikaji na tija katika taaluma ya uandishi wa habari.


.jpeg)
Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050 ya kujenga Tanzania yenye uchumi wa kisasa, jamii yenye ustawi, huduma bora za kijamii pamoja na matumizi makubwa ya teknolojia na ubunifu, imeelezwa kuwa inahitaji Serikali za Mitaa imara, zenye uwezo na zinazowajibika ili kuhakikisha malengo hayo yanafikiwa kwa ufanisi na kwa usawa.
Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Dkt. Jafar Seif, amesema ugatuzi wa madaraka katika mamlaka za Serikali za Mitaa ni nyenzo muhimu ya kufanikisha Dira hiyo, kwa kuwa unawawezesha wananchi kushiriki kikamilifu katika maamuzi na utekelezaji wa shughuli za maendeleo katika maeneo yao.
Dkt. Seif ameyasema hayo leo jijini Dodoma wakati akifungua Mkutano Mkuu wa 16 wa Taasisi ya Maboresho katika Mamlaka za Serikali za Mitaa (TOA), unaofanyika chini ya kaulimbiu isemayo “Ugatuzi wa Madaraka katika Mamlaka za Serikali za Mitaa ni Nyenzo Madhubuti ya Kufikia Dira ya Taifa 2050.”
Amesema ugatuzi wa madaraka si suala la kiutawala pekee, bali ni msingi wa kuwapa wananchi nafasi ya kushiriki katika maamuzi yanayohusu maendeleo yao, akieleza kuwa Serikali za Mitaa ndizo zilizo karibu zaidi na wananchi na zina nafasi kubwa katika kuhakikisha huduma na miradi ya maendeleo inawafikia kwa wakati.
“Serikali za Mitaa zikiwa imara na zenye uwezo wa kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi, Taifa linaweza kufikia malengo yake kwa haraka zaidi na kwa usawa,” amesema Dkt. Seif.
Amesema Serikali imepanga kuchukua hatua zaidi katika eneo la ugatuzi wa madaraka kwa kuimarisha mifumo mbalimbali ya kiutendaji na usimamizi, hususan katika eneo la fedha, hatua inayolenga kuongeza ufanisi wa utekelezaji wa miradi na utoaji wa huduma kwa wananchi.
Dkt. Seif amesema kwa sasa fedha za utekelezaji wa miradi ya maendeleo zinapelekwa moja kwa moja katika taasisi za Serikali zilizopo ngazi za chini, ikiwemo shule, zahanati, ofisi za kata, vijiji pamoja na maeneo mengine ya kiutawala na kiutendaji.
Ameeleza kuwa hatua hiyo inalenga kuhakikisha rasilimali zinazotengwa kwa ajili ya maendeleo zinawafikia walengwa moja kwa moja na kutumika katika kutatua changamoto zinazowakabili wananchi katika maeneo yao.
Aidha, Dkt. Seif amesema ili Dira ya Taifa ya 2050 ifikiwe, Serikali za Mitaa zinapaswa kuimarisha maeneo muhimu ikiwemo uongozi bora na uwajibikaji, mipango madhubuti ya maendeleo, usimamizi wa rasilimali za umma, ushirikishwaji wa wananchi pamoja na matumizi ya TEHAMA katika utoaji wa huduma.
Amesema TOA imeendelea kuwa jukwaa muhimu la kuwakutanisha viongozi na wataalamu wa Serikali za Mitaa kwa ajili ya kubadilishana uzoefu, kujifunza na kutafuta suluhisho la changamoto zinazojitokeza katika ngazi za chini za utendaji.
Dkt. Seif amesisitiza kuwa mafanikio ya ugatuzi wa madaraka yanategemea kwa kiasi kikubwa uwezo wa taasisi kujenga mazingira ya uwazi, uwajibikaji na ushirikiano katika utekelezaji wa majukumu ya Serikali za Mitaa.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa TOA, Albert Msovela, amesema taasisi hiyo itaendelea kushirikiana na Serikali katika kusimamia maendeleo ya wananchi na kuimarisha utawala bora, huku akisisitiza umuhimu wa kuendelea kujenga uwezo wa mamlaka za Serikali za Mitaa ili ziweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi.
Mkutano huo wa 16 wa TOA unajadili masuala mbalimbali yanayohusu maboresho ya utendaji wa Serikali za Mitaa, ugatuzi wa madaraka na namna ya kuimarisha utoaji wa huduma kwa wananchi katika kuelekea utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050.





.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)


.jpeg)

















.jpeg)



.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)




.jpeg)

.jpeg)



.jpeg)
