Na Mwandishi Wetu, Tanga
SERIKALI imesema mashindano ya ujuzi na ubunifu ni sehemu ya mkakati wa kuwaandaa vijana wenye ujuzi unaokidhi mahitaji ya soko la ajira na kuwawezesha kushindana katika majukwaa ya kimataifa.

Hayo ameyasema Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Carolyne Nombo, wakati akizungumza katika Wiki ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu inayoendelea jijini Tanga.

Profesa Nombo amesema Serikali imekuwa ikitumia mbinu mbalimbali kuwawezesha vijana kupata ujuzi, ikiwemo kuwatoa darasani na kuwapeleka katika maeneo halisi ya kazi pamoja na kuwashirikisha katika mashindano yanayopima uwezo na umahiri wao.

Amesema Tanzania baada ya kuwa mwanachama wa mashindano ya WorldSkills, imeanza mchakato wa kuwachagua vijana wenye ujuzi kuanzia ngazi za chini hadi mashindano ya kitaifa, ambapo watakaofanya vizuri wataiwakilisha nchi katika mashindano ya Afrika yanayotarajiwa kufanyika mwaka huu nchini Algeria.

“Tunapotaka kuhamasisha vijana kupata ujuzi, tunatumia mbinu mbalimbali zaidi ya kuwafundisha darasani. Tunataka vijana hawa waende katika maeneo halisi ya kazi ili wapate ujuzi unaotakiwa,” amesema Profesa Nombo.

Amesema vijana wanaoshiriki mashindano hayo wamechaguliwa baada ya kuonyesha umahiri katika fani mbalimbali, huku wataalamu wakifanya tathmini kwa kuzingatia viwango vya kimataifa ili kubaini watakaoiwakilisha Tanzania katika mashindano ya Afrika na baadaye ya dunia.

Profesa Nombo amesema Serikali inalenga kuhakikisha vijana wa Tanzania wanapata fursa ya kuonyesha uwezo wao na kuifanya dunia itambue kuwa nchi ina vijana wenye ujuzi na ubunifu unaoweza kushindanishwa katika majukwaa ya kimataifa.

Amesema Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (NACTVET) limeratibu mashindano hayo kwa kushirikisha wataalamu kutoka ndani na nje ya nchi.

Kwa mujibu wa Profesa Nombo, wataalamu wa Wizara ya Elimu na wadau wengine wamepatiwa mafunzo na wataalamu wa kimataifa kuhusu namna mashindano ya WorldSkills yanavyoendeshwa ili kuhakikisha Tanzania inazingatia vigezo vya kimataifa.

Amesema pia viongozi na wataalamu wa Tanzania watashiriki katika kujifunza namna mashindano ya kimataifa yanavyoandaliwa na kuendeshwa, hatua ambayo itasaidia kuboresha zaidi maandalizi ya timu ya taifa.

Profesa Nombo amesema kinachofurahisha katika mashindano hayo ni ushirikiano unaoendelea kati ya taasisi za elimu, vyuo vya ufundi, viwanda na sekta binafsi katika kuwaandaa vijana.

Amesema wataalamu kutoka sekta binafsi na taasisi mbalimbali wamekuwa wakishirikiana na vyuo kutoa maarifa na uzoefu kwa vijana ili kuwawezesha kufanya vizuri katika mashindano hayo.

“Tunakwenda kwenye mashindano haya kama Tanzania iliyounganika kati ya sekta ya umma na sekta binafsi. Lengo ni kuhakikisha tunashiriki kama timu moja ya Tanzania,” amesema.

Amesema ushirikiano huo ni muhimu kwa kuwa unawawezesha wanafunzi kupata uzoefu wa vitendo na ujuzi unaoendana na mahitaji ya soko la ajira.

Aidha, Profesa Nombo amesema Serikali imeweka mkazo katika elimu jumuishi kwa kuhakikisha vijana wote wanapata fursa ya kutumia vipaji na uwezo wao bila kujali changamoto walizonazo.

Amesema vijana wenye mahitaji maalum wamepewa nafasi ya kushiriki katika mashindano hayo na kuonyesha uwezo wao katika fani mbalimbali.

“Ushiriki wa vijana wenye mahitaji maalum unaonyesha wazi kuwa hata wenye changamoto hizo wanaweza kuwa na mchango mkubwa katika maisha yao na katika maendeleo ya taifa,” amesema.

Amesisitiza kuwa Serikali itaendelea kutoa fursa kwa vijana wote, wakiwemo wenye mahitaji maalum, ili waweze kujenga maisha yao na kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya Taifa.


Na Mwandishi Wetu
WADAU wa teknolojia na usimamizi wa intaneti wametakiwa kutumia fursa zinazotokana na mtandao huo kwa maendeleo ya jamii badala ya kuutumia kwa matusi, chuki, udhalilishaji na vitendo vinavyoweza kuathiri maslahi na haki za watu wengine.

Rai hiyo imetolewa na Mratibu wa Tanzania Internet Governance Forum (TIGF), Dkt. Nazarius Kirama, wakati wa Mkutano wa 13 wa Jukwaa la Usimamizi wa Intaneti Tanzania, unaojadili masuala mbalimbali yanayohusu matumizi, usalama na mustakabali wa intaneti nchini.

Kirama amesema mkutano huo umewakutanisha wadau kutoka serikalini, mashirika yasiyo ya kiserikali, sekta binafsi, wataalamu na wasomi kutoka vyuo vikuu kwa lengo la kujadili namna ya kukuza matumizi salama na yenye tija ya intaneti, huku masuala ya akili mnemba (AI), ujumuishi wa kidijitali, ulinzi wa taarifa binafsi na intaneti yenye kasi yakiwa miongoni mwa mada zinazojadiliwa.

Amesema Jukwaa la Usimamizi wa Intaneti Tanzania lilianza mwaka 2005 na ni sehemu ya mfumo wa mijadala ya usimamizi wa intaneti unaofanyika katika ngazi za kitaifa, kikanda na kimataifa, uliolenga kutoa nafasi kwa wadau kujadili namna bora ya kusimamia mustakabali wa teknolojia hiyo.

Kirama amesema licha ya intaneti kuwa nyenzo muhimu ya kufikisha huduma, taarifa na fursa kwa watu wengi, baadhi ya watumiaji wamekuwa wakiitumia vibaya kwa kutoa lugha za matusi, chuki na vitendo vinavyoweza kuharibu maslahi ya wengine, akisema tabia hizo zinaakisi changamoto zilizopo katika jamii.

“Jamii iliyopo kwenye mitandao ya kijamii haikutoka mbinguni, inatokana na jamii yetu. Kwa hiyo yale mambo yanayofanyika mtaani yanaweza pia kufanyika mtandaoni,” amesema Kirama, huku akiwataka watumiaji kujenga utamaduni wa kujidhibiti badala ya kutegemea udhibiti wa mamlaka pekee.

Amesema wananchi wanapaswa kutafakari thamani wanayoipata kutokana na matumizi ya intaneti na kuhakikisha fedha wanazolipia huduma hiyo zinatumika kwa shughuli zenye manufaa, ikiwamo kujenga jamii, kuelimisha, kuongeza fursa za kiuchumi na kuunganisha watu. “Intaneti ya bure bila faida ni kujiletea umaskini.

Kwa nini utumie fedha kulipia intaneti halafu uitumie kumtukana mtu? Intaneti yenyewe ina gharama,” amesema.

Katika mkutano huo, Mwanaharakati wa masuala ya teknolojia na miundombinu ya TEHAMA, Damilola Kihinde, amewataka wazazi, hospitali na wahusika wengine wanaokusanya au kuhifadhi taarifa za watoto kuhakikisha taarifa hizo zinalindwa ili kuepusha matumizi mabaya, udhalilishaji na uvunjwaji wa haki zao za msingi.

Kihinde amesema mtoto mdogo hawezi kufanya maamuzi kuhusu matumizi ya taarifa zake, hivyo mzazi akiwa mlezi na mlinzi wake wa kwanza ana wajibu wa kuhakikisha picha na taarifa zake hazishirikishwi au kutumiwa kwa namna inayoweza kumletea madhara.

Amesema pia hospitali, ambazo zinaweza kuwa wadhibiti wa taarifa kwa mujibu wa Sheria ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi, zinapaswa kuweka mifumo imara ya kulinda taarifa za watoto na wagonjwa.

Amesisitiza kuwa ulinzi wa taarifa binafsi za watoto ni jukumu la pamoja linalohitaji ushirikiano wa wazazi, hospitali na wahusika wengine, huku maslahi bora ya mtoto na haki yake ya faragha yakipewa kipaumbele.

Kwa upande wake, Pious Sylvester, Mratibu wa Ushirikiano wa Shirika la African Child Project, amesema jamii inapaswa kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa kulinda taarifa za watoto, hasa katika kipindi ambacho matumizi ya mitandao ya kijamii yanaendelea kuongezeka.

Amesema Tanzania pia inapaswa kuendelea kushiriki katika majukwaa ya kikanda na kimataifa kuhusu usimamizi wa intaneti ili kupata fursa ya kujadili changamoto na kutoa mchango katika mijadala ya mustakabali wa teknolojia.




Mkuu wa Chuo cha Bahari Dar es Salaam (DMI), Prof. Tumaini Gurumo, amesema maandalizi ya Kongamano la 5 la Kimataifa la Uchumi wa Buluu yanaendelea vizuri. Kongamano hilo linatarajiwa kufanyika tarehe 7 hadi 9 Septemba 2026 katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNICC), Dar es Salaam, huku washiriki kutoka zaidi ya nchi saba wakitarajiwa kuhudhuria.

Akizungumza na waandishi wa habari leo tarehe 20 Agosti 2026, katika Ukumbi wa Mikutano wa DMI, Prof. Gurumo amesema kongamano hilo limeandaliwa na DMI, chini ya Wizara ya Uchukuzi, kwa kushirikiana na Ofisi ya Makamu wa Rais, likiwa na kaulimbiu “Kuwezesha Shughuli za Uchumi wa Buluu kwa Maendeleo Endelevu ya Afrika.” Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, anatarajiwa kuwa Mgeni Rasmi.

Prof. Gurumo amesema kongamano hilo linafanyika wakati Tanzania ikiendelea na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, huku utajiri wa Bahari ya Hindi, maziwa, mito, visiwa na rasilimali nyingine za maji yakiwa na fursa kubwa katika kuchochea uwekezaji, biashara, ajira, usalama wa chakula, usafiri, utalii, nishati, utafiti na teknolojia.

Ameeleza kuwa kongamano litakuwa jukwaa la kuunganisha tafiti, maarifa, sera, teknolojia na wadau mbalimbali katika kujadili fursa, changamoto na suluhisho za matumizi ya rasilimali za Uchumi wa Buluu kwa maendeleo endelevu. Msisitizo utawekwa katika utafiti na ushahidi wa kisayansi, uwekezaji, ushiriki wa sekta binafsi na wananchi, ubunifu na kujenga uwezo wa kitaasisi, kwa kuzingatia Sera ya Taifa ya Uchumi wa Buluu ya mwaka 2024.

Katika kongamano hilo, wataalamu, watafiti na wanazuoni wanatarajiwa kuwasilisha tafiti na kubadilishana uzoefu katika maeneo mbalimbali, yakiwemo bandari na usafiri wa majini, mazingira ya bahari, mabadiliko ya tabianchi, uvuvi na ufugaji wa viumbe vya majini, sheria za bahari, teknolojia, ujasiriamali, elimu na mafunzo ya bahari, usalama wa bahari na uwekezaji.

Prof. Gurumo amesema kongamano linatarajiwa kuwakutanisha washiriki kutoka Tanzania na mataifa mbalimbali, yakiwemo China, Afrika Kusini, Sweden, Japan, Canada, Russia, Thailand, Morocco, Kenya, Comoro na Uturuki, kwa ajili ya kubadilishana maarifa, teknolojia na uzoefu, pamoja na kuimarisha ushirikiano wa kitaifa, kikanda na kimataifa katika kukabiliana na changamoto za bahari.

Kwa upande wa DMI, Prof. Gurumo amesema kongamano hilo ni sehemu ya jukumu la Chuo la kuwa kitovu cha elimu, mafunzo, utafiti na ubunifu katika sekta ya bahari na Uchumi wa Buluu. Kongamano linatarajiwa kutoa maarifa mapya, mapendekezo ya kisera yanayotokana na ushahidi wa kisayansi, fursa za utafiti na ushirikiano wa kitaaluma na kitaasisi, pamoja na fursa za ubunifu na uwekezaji.

Mkuu wa Chuo cha Bahari Dar es Salaam (DMI), Prof. Tumaini Gurumo, amewakaribisha wataalamu, watafiti, wanazuoni, wawakilishi wa sekta binafsi, wawekezaji, taasisi za kitaifa na kimataifa, wadau wa maendeleo pamoja na jumuiya ya kitaaluma kushiriki katika Kongamano la 5 la Kimataifa la Uchumi wa Buluu, linaloandaliwa na DMI kwa kushirikiana na Ofisi ya Makamu wa Rais na Wizara ya Uchukuzi.




Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Elimu, Utamaduni na Michezo, Mheshimiwa Husna Sekiboko, ametoa wito wa kuimarishwa kwa elimu na mafunzo ya ufundi na ujasiriamali nchini, akisema ujuzi wa vitendo unaweza kuwa silaha muhimu kwa vijana katika kukabiliana na ukosefu wa ajira kwa kujiajiri na kuunda ajira kwa wengine.

Amesema hayo akiwa kwenye banda la VETA katika Maadhimisho ya Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu, Jijini Tanga.

Sekiboko amesema badala ya vijana kuhitimu na kuendelea kusubiri ajira, wanapaswa kutumia ujuzi wanaoupata katika vyuo vya ufundi kuanzisha shughuli za uzalishaji, huku Serikali ikiendelea kuweka mazingira ya kuwawezesha kupata vitendea kazi, mitaji na masoko.

Amesema changamoto ya ukosefu wa ajira inahitaji suluhisho linalowafanya vijana kuwa sehemu ya uzalishaji, akisisitiza kuwa kijana mwenye ujuzi ana uwezo wa kujiajiri na baadaye kuwa mwajiri wa wengine.

“Ni bora kijana kuanza na kile kidogo alichonacho na kujenga shughuli yake mwenyewe, kwa sababu anaweza kujiajiri na baadaye kuajiri wengine. Kwa kufanya hivyo, anakuwa amefanya zaidi kwa ajili yake mwenyewe na jamii yake kuliko kusubiri ajira pekee,” amesema.

Ametoa kauli hiyo baada ya kutembelea banda la VETA na kukutana na vijana na wanachuo na wahitimu wa VETA ambapo amesema ameona uwezo mkubwa walionao katika kutengeneza bidhaa na kutoa huduma zinazoweza kukidhi mahitaji ya jamii.

Kwa mujibu wa Sekiboko, vyuo vya ufundi stadi vina nafasi kubwa katika utekelezaji wa jitihada za kukabiliana na ukosefu wa ajira kwa sababu vinawapatia vijana ujuzi wa vitendo ambao unaweza kutumika moja kwa moja katika uzalishaji.

Amesema ili ujuzi huo uwe na matokeo makubwa zaidi, vijana wanahitaji mazingira mazuri ya kujifunzia, vifaa vya kufanyia kazi na fursa za kupata mitaji ili kugeuza ujuzi wao kuwa biashara na ajira.

Amehimiza vijana kutumia fursa zinazotolewa na Serikali na taasisi mbalimbali kupata ujuzi na mitaji, akisema mtaji mdogo unaweza kuwa mwanzo wa shughuli kubwa endapo utatumika vizuri.

“Lengo ni kuondokana na utamaduni wa kusubiri ajira pekee. Kijana akipata ujuzi, anaweza kuutumia kuzalisha ajira yeye mwenyewe badala ya kusubiri kuajiriwa katika taasisi,” amesema.

Amesema hatua hiyo pia inaweza kusaidia kufikia malengo ya Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 kwa kuongeza idadi ya vijana wanaoshiriki katika uzalishaji na kujenga uchumi kupitia ujuzi, ubunifu na ujasiriamali.









Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Nombo, ameiagiza Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania (TAEC) kuongeza elimu kwa umma kuhusu matumizi ya teknolojia ya nyuklia, ili Watanzania waelewe manufaa yake na matumizi chanya katika maisha na maendeleo ya taifa.

Prof. Nombo ametoa agizo hilo Agosti 20, 2026 jijini Tanga alipotembelea banda la TAEC katika Maonesho ya Wiki ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu Kitaifa yanayofanyika katika viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara kuanzia Agosti 15 hadi 24.

Amesema elimu hiyo ni muhimu katika kuondoa hofu na dhana potofu kuhusu teknolojia ya nyuklia, huku akisisitiza umuhimu wa kuwajengea wananchi uelewa kuhusu matumizi yake katika sekta mbalimbali.

Prof. Nombo amewataka wataalamu wa TAEC kuendelea kujenga uwezo wa wataalamu wengine wa ndani, ili Tanzania iwe na rasilimali watu wenye ujuzi wa kutosha wa kutumia na kuendeleza teknolojia ya nyuklia kwa manufaa ya taifa.

Ameeleza kuwa serikali imeendelea kutoa fursa za masomo na ufadhili (scholarship) kwa Watanzania wanaosomea fani zinazohusiana na teknolojia ya nyuklia, hatua inayolenga kuongeza idadi ya wataalamu wenye ujuzi na kujenga uwezo wa nchi katika eneo hilo.

Aidha, Prof. Nombo amesema Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, anatarajiwa kushiriki katika mkutano wa kimataifa unaohusisha masuala ya teknolojia ya nyuklia ambayo ni ishara ya umuhimu na fursa ya Tanzania kuimarisha ushirikiano na nchi nyingine katika sekta hiyo.

Akizungumza baada ya kupokea maelekezo hayo, Mtafiti Mwandamizi kutoka TAEC, Eng. Christina Paul Nyakyi, amesema taasisi hiyo imepokea maelekezo hayo na itayafanyia kazi kwa kuongeza juhudi za kutoa elimu kwa wananchi kuhusu matumizi salama ya teknolojia ya nyuklia.

Amesema TAEC itaendelea kuweka mkazo katika matumizi ya teknolojia hiyo kwa maendeleo ya taifa, pamoja na kuwaandaa wataalamu wa ndani watakaoweza kushiriki katika matumizi na uendelezaji wa teknolojia ya nyuklia nchini.




 NA EMMANUEL  MASSAKA 

 
MAMLAKA ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA) imeshauriwa kuendelea kuimarisha utoaji wa elimu kwa wananchi kuhusu matumizi sahihi ya dawa na vifaa tiba.Ushauri huo umetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Bi. Queen Sendiga alipokuwa akifungua kikao cha siku mbili kati ya TMDA, wahariri na waandishi wa habari kutoka mikoa ya Manyara, Arusha na Kilimanjaro, kilichofanyika mkoani Manyara.


Lengo la kikao hicho ni kwa kuwajengea uelewa kuhusu majukumu ya TMDA, udhibiti wa dawa, vifaa tiba na vitendanishi pamoja na changamoto zinazojitokeza katika eneo hilo.

Ametumia nafasi hiyo kueleza kuwa taarifa sahihi kuhusu bidhaa za tiba ni muhimu kwa sababu sekta hiyo inahusisha moja kwa moja afya na mustakabali wa jamii, hivyo wananchi wanapaswa kupata taarifa sahihi na kwa wakati ili waweze kufanya maamuzi salama.

Mkuu wa Mkoa huyo amesema wanapozungumzia bidhaa za tiba wanazungumzia afya na mustakabali wa jamii yetu kwa ujumla. Hivyo ni muhimu wananchi wapate taarifa sahihi kuhusu dawa na vifaa tiba.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Dawa za Binadamu na Mifugo wa TMDA, Dkt. Yona Mwalwisi, amesema mamlaka hiyo inaendelea kutekeleza majukumu yake kwa mujibu wa Sheria ya Dawa na Vifaa Tiba, Sura ya 219, inayoiwezesha kusimamia ubora, usalama na ufanisi wa dawa, vifaa tiba na vitendanishi nchini.

“TMDA imejenga utamaduni wa kukutana na wahariri na waandishi wa habari kila mwaka katika maeneo mbalimbali nchini ili kujadili mafanikio, changamoto na mikakati ya pamoja ya kuboresha udhibiti wa bidhaa za tiba na kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu huduma zinazotolewa na mamlaka hiyo.”

Ameongeza utafiti wa kuridhika kwa wananchi na wateja uliofanywa na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, hususan Shule ya Biashara Desemba 2022 katika halmashauri 35 za mikoa 16, umeonesha kuongezeka kwa uelewa kuhusu TMDA kutoka asilimia 47 mwaka 2020, huku kiwango cha kuridhika na huduma za mamlaka hiyo kikiwa asilimia 82.

“Mafanikio hayo yamechangiwa kwa kiasi kikubwa na ushirikiano kati ya TMDA na vyombo vya habari, ambavyo vimekuwa daraja muhimu la kufikisha elimu kwa wananchi kuhusu matumizi sahihi ya dawa na vifaa tiba, pamoja na kuwaelimisha kuhusu hatari za bidhaa bandia, duni na zisizosajiliwa.”

Aidha, amesema TMDA imeendelea kushikilia cheti cha mfumo wa usimamizi wa ubora ISO 9001:2015 pamoja na ithibati ya maabara kwa kiwango cha ISO 17025:2017, jambo linalothibitisha kuwa mifumo na huduma zinazotolewa na mamlaka hiyo zinakidhi viwango vya kimataifa.

Amesema TMDA pia imetambuliwa na Shirika la Afya Duniani (WHO) kuwa mamlaka iliyofikia ngazi ya tatu ya ukomavu wa mifumo ya udhibiti wa bidhaa za tiba, huku ikiendelea na juhudi za kufikia ngazi ya nne, ambayo ndiyo ya juu zaidi, na kuendelea kuwa miongoni mwa mamlaka zinazoongoza barani Afrika.

Pamoja na hayo ameeleza mamlaka hiyo imeimarisha ufuatiliaji wa usalama wa dawa na chanjo baada ya kuingia sokoni, ikiwa ni pamoja na kuongeza vituo vya kufuatilia madhara ya dawa na chanjo hadi kufikia vituo 33 nchini.

Aiidha mtandao wa maabara hamishika ukiongezeka kutoka 19 hadi 28, hatua inayowezesha upimaji wa sampuli katika maeneo mbalimbali kwa wakati. TMDA pia imeweka vituo vya maabara katika vituo vyote 16 rasmi vya forodha vinavyoingiza bidhaa za tiba nchini.



























Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Msanii Mkongwe kutoka nchini Afrika ya Kusini Yvonne Chakachaka, tarehe 20 Agosti, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam.

Msanii huyo yupo nchini kwa ajili ya kushiriki katika Jukwaa la Mashariki Creative Expo 2026 likiwa na lengo la kutoa elimu na ulinzi kwenye kazi za ubunifu zinazojumuisha filamu, sanaa za ufundi na muziki.











Chuo cha Mipango ya Maendeleo Vijijini (IRDP) kimeonyesha ubunifu katika teknolojia, upangaji wa ardhi na ujasiriamali, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kutumia elimu na tafiti kutatua changamoto zinazowakabili wananchi.

Akizungumza Agosti 19, 2026, katika Wiki ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu inayoendelea Jijini Tanga, Mkuu wa Chuo Cha Mipango Profesa Hozen Mayaya, amesema chuo hicho kimekuja kuonyesha bunifu mbalimbali zinazofanywa na wanafunzi ili kuisaidia jamii.

Amesema chuo hicho kina kampasi mbili ambazo ni Dodoma na Mwanza, na kinafundisha vijana masuala ya TEHAMA , ambapo baadhi yao mwanafunzi amebuni mfumo unaolenga kusaidia kuboresha huduma katika sekta ya afya na Benki kwa kuondoa foleni na kumsaidia mteja kufahamu muda wa kupata huduma na kuondoa upendeleo.

Aidha, ameeleza kuwa wanatoa mafunzo ya upangaji wa ardhi, miji na vijiji, akisisitiza umuhimu wa kuwaandaa wataalamu watakaokabiliana na changamoto za ukuaji wa makazi.

“Tunafundisha masuala ya upangaji miji pamoja na upangaji wa vijiji, kwa sababu tunaamini vijiji vya leo ni miji ya kesho,” amesema.

Amesema kupitia programu ya Mipango Planning, Entrepreneurship and Innovation Centre MEI wanafunzi wanapata fursa ya kutumia maarifa wanayopata darasani kutengeneza bidhaa zinazoweza kuingia sokoni, ikiwemo sabuni, vinywaji na bidhaa nyingine.

Kwa upande mwingine, amesema wanaendelea kushirikiana na jamii, hususan vikundi vya wanawake na wajasiriamali wa vijijini, kwa kuwapatia elimu na ushauri wa namna ya kutumia rasilimali walizonazo kuanzisha na kukuza biashara.

Aidha, amebainisha majukumu makuu ya chuo hicho ni kufundisha, kufanya utafiti na kutoa huduma za kitaalamu kwa jamii, huku kikitenga bajeti kwa ajili ya tafiti zinazolenga kutatua changamoto za maendeleo kwenye jamii.

Profesa Mayaya ameeleza namna chuo hicho kinajivunia watafiti wake watatu, ambao ni Profesa Provident Dimoso, Dkt. Rwezaula na Dkt. Biaro, waliotambuliwa kwa kufanya utafiti bora kupitia tuzo iliyotolewa na Wizara ya elimu ya chapisho bora lenye hadhi ya juu Duniani, akisema mafanikio hayo yanaongeza hamasa kwa watafiti wengine kuendelea kuzalisha tafiti zenye manufaa kwa jamii.

Amesema chuo kitaendelea kuwekeza katika elimu, utafiti na ubunifu ili kuhakikisha maarifa yanayozalishwa chuoni yanatumika katika kutatua changamoto na kuchochea maendeleo ya wananchi, hususan katika maeneo ya vijijini.


Na Belinda Joseph-Tanga

Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) inatekeleza Mradi wa Elimu na Stadi kwa Ajira zenye Tija Awamu ya Pili (ESPJ II), unaolenga kuimarisha mafunzo ya ufundi stadi nchini kupitia uanzishaji wa vituo 15 vya umahiri katika maeneo mbalimbali.

Akizungumza katika Wiki ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu, Meneja Uhusiano na Masoko kutoka VETA Sitta Peter, amesema mradi huo ni sehemu ya hatua za Mamlaka hiyo kupanua mafunzo ya ufundi stadi na kuhakikisha vijana wanapata ujuzi unaoendana na mahitaji ya soko la ajira.

Amesema vituo hivyo vitajikita katika maeneo maalumu ya mafunzo na umahiri, hatua inayolenga kuongeza ubora wa mafunzo na kuwaandaa wahitimu wenye uwezo wa kufanya kazi kwa viwango vinavyohitajika katika sekta mbalimbali kwenye soko la ajira kimataifa.

Amewahimiza wananchi kutumia fursa ya maonesho ya Wiki ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu kutembelea banda la VETA na kupata taarifa kuhusu kozi zinazotolewa, hasa kwa kuwa maombi ya mafunzo ya muda mrefu yanaendelea kupokelewa.

Amesema VETA ni kwa ajili ya Watanzania wote yaani wenye viwango tofauti vya elimu, kuanzia waliomaliza elimu ya msingi hadi wenye shahada na shahada za uzamili, hivyo wananchi wanapaswa kuchagua stadi wanayoona inaweza kuwasaidia katika ajira au kujiajiri.

Ameeleza kuwa gharama za mafunzo ni nafuu, ambapo mwanafunzi wa kutwa hulipa shilingi 60,000 kwa mwaka, huku anayekaa bweni akilipa shilingi 120,000 kwa mwaka, bila kujumuisha baadhi ya mahitaji binafsi na vifaa vya usalama vinavyohitajika katika mafunzo ya vitendo.

Aidha, Sitta amewahimiza watu wenye ulemavu kuchangamkia fursa hiyo, kwa kuwa wanafunzi wenye ulemavu wanaodahiliwa kujiunga na VETA wanalipiwa malipo ya ada na Mamlaka hiyo, hivyo wao wanatakiwa kugharamia mahitaji yao binafsi na sio ada.


NA DENIS MLOWE IRINGA


MEYA wa Manispaa ya Iringa, Ibrahim Ngwada, amefuta taarifa iliyokuwa imeeleza kuwa Halmashauri imekubaliana kuongeza ada katika shule za mchepuo wa Kiingereza, ikiwemo Shule ya Msingi Mapinduzi, kutoka Shilingi 300,000 hadi Shilingi 500,000 kwa mwaka.

Akizungumza katika kikao cha Baraza la Madiwani la Halmashauri ya Manispaa ya Iringa, Meya Ngwada alisema suala la kuongeza ada halijapitishwa na kwamba kumbukumbu zilizowasilishwa zilikuwa na taarifa isiyoendana na uamuzi wa kikao.

Alisema awali wataalamu walipewa jukumu la kufanya upembuzi na kuwasilisha mapendekezo kuhusu uwezekano wa kubadili ada, na kwamba suala hilo linapaswa kurejea katika vikao halali vya kisheria kabla ya uamuzi wowote kufanyika.

“Hatujapandisha ada kwenye shule zetu za Mapinduzi, Gangilonga na Chifu Mkwawa. zitabaki kuwa zile zile hatujabadilisha ada,” alisema Meya Ngwada.

Meya Ngwada aliwataka wazazi na wananchi kutokuwa na hofu, akisisitiza kuwa kwa sasa hakuna ongezeko la ada lililoidhinishwa katika shule hizo na endapo kutakuwa na umuhimu wa kufanya mabadiliko, suala hilo litajadiliwa na kuamuliwa kupitia taratibu za kisheria.

Baraza hilo pia lilijadili hoja kuhusu uamuzi wa kuhamisha Shule ya Msingi Ilala kuwa chini ya Chuo Kikuu cha Mkwawa ambapo Meya Ngwada alisema uamuzi huo umempa maswali, hasa baada ya kupata maelezo kuwa pamoja na shule hiyo, ardhi ilipojengwa pia itahamishwa.

Alisema Chuo Kikuu cha Mkwawa kina eneo kubwa linalozidi ekari 600, hivyo kwa mtazamo wake kungekuwa na uwezekano wa kutenga eneo ndani ya chuo hicho na kujenga shule mpya badala ya kuhamisha ardhi ya shule hiyo kutoka katika umiliki wa Halmashauri.

Meya Ngwada alisisitiza kuwa hoja yake haikuwa ya kupinga uamuzi ambao tayari umepitishwa na vikao vya Halmashauri, bali alikuwa akiweka wazi wasiwasi wake kuhusu umiliki wa ardhi na namna rasilimali hiyo inavyoweza kutumika kwa manufaa ya wananchi

Kwa upande mwingine, Diwani Likotiko Kenyatta alihoji utekelezaji wa mpango wa Halmashauri wa kufanya mazungumzo na Chama Cha Mapinduzi kuhusu eneo la Sabasaba.

Akijibu hoja hiyo, Ngwada alileza kuwa eneo hilo linamilikiwa na Chama Cha Mapinduzi na lina hati ya umiliki halmashauri imependekeza kufanyika kwa mabadilishano ya maeneo ili eneo hilo liweze kubaki chini ya matumizi ya wananchi.

Eneo la Sabasaba lina Shule ya Msingi, shule ya mahitaji maalum pamoja na kituo cha afya, hivyo Halmashauri imesema inaona umuhimu wa kupata umiliki wa eneo hilo ili iweze kuendelea kufanya uwekezaji katika huduma hizo.







Top News