Na Janeth Raphael -MichuziTv
Tanzania na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) zimeweka mkazo mpya katika kuimarisha uhusiano wao wa kiuchumi na kimkakati, huku sekta za madini, biashara, uwekezaji na miundombinu zikitajwa kuwa maeneo muhimu ya ushirikiano kati ya mataifa hayo mawili.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema hayo leo Agosti 18, 2026, Ikulu Ndogo Zanzibar, baada ya kumpokea Rais wa DRC, Félix Antoine Tshisekedi Tshilombo, aliyewasili nchini kwa ziara ya kikazi.
Rais Samia amesema mazungumzo yake na Rais Tshisekedi yamejikita katika namna Tanzania na DRC zinavyoweza kutumia fursa zilizopo katika rasilimali na uchumi wa mataifa hayo kwa manufaa ya wananchi wa nchi zote mbili.
Kwa mujibu wa Rais Samia, sekta ya madini ni miongoni mwa maeneo yenye nafasi kubwa ya kuunganisha Tanzania na DRC, kutokana na utajiri wa rasilimali za madini uliopo katika nchi hizo.
Amesema ushirikiano huo unaweza kuwezesha mataifa hayo kubadilishana uzoefu na utaalamu katika uchimbaji wa madini, uongezaji thamani pamoja na upatikanaji wa masoko, hatua inayoweza kuongeza mchango wa sekta hiyo katika uchumi wa nchi zote mbili.
Katika eneo la biashara na uwekezaji, Rais Samia amesema Tanzania na DRC zimekubaliana kuweka mazingira yatakayorahisisha zaidi shughuli za wafanyabiashara na wawekezaji, ikiwemo kupunguza vikwazo visivyo vya lazima na kuboresha huduma katika maeneo ya mipakani.
Amesema hatua hiyo inalenga kuongeza mzunguko wa bidhaa na huduma kati ya nchi hizo, huku sekta binafsi ikipewa nafasi kubwa zaidi ya kutumia fursa zinazotokana na ushirikiano huo.
Miundombinu pia imepewa uzito katika mazungumzo hayo, ambapo Rais Samia amesema kukamilika kwa ujenzi wa barabara ya Kalemie–Manono kutakuwa na umuhimu mkubwa katika kuimarisha muunganiko wa Tanzania na DRC.
Amesema miundombinu hiyo haitarahisisha tu usafirishaji wa watu na bidhaa, bali pia itafungua zaidi fursa za biashara na kuchochea shughuli za kiuchumi katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.
Mbali na masuala ya kiuchumi, viongozi hao wamezungumzia pia amani na usalama, huku wakisisitiza umuhimu wa ushirikiano katika kulinda utulivu wa eneo la Afrika na kuweka mazingira bora kwa maendeleo ya wananchi.
Rais Samia amesema Tanzania itaendelea kuwa mshirika wa karibu wa DRC katika juhudi za kujenga uchumi unaowaunganisha wananchi wa mataifa hayo, pamoja na kuendeleza mazingira yatakayowezesha biashara, uwekezaji na maendeleo ya pamoja.
Amesema ziara ya Rais Tshisekedi nchini Tanzania ni fursa ya kuendeleza uhusiano wa kihistoria uliopo kati ya nchi hizo na kuufanya kuwa msingi wa ushirikiano mpana zaidi katika maeneo ya kimkakati.
Kwa hatua hiyo, Tanzania na DRC zimeelekeza nguvu katika kujenga ushirikiano unaokwenda zaidi ya mahusiano ya kidiplomasia, kwa kulenga kuunganisha uchumi, miundombinu, biashara na fursa za uwekezaji kwa manufaa ya wananchi wa pande zote mbili.
Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) Mhe. Félix Antoine Tshisekedi Tshilombo akisaini Kitabu cha Wageni baada ya kuwasili Ikulu Ndogo ya Zanzibar, tarehe 18 Agosti, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) Mhe. Félix Antoine Tshisekedi Tshilombo baada ya kuwasili Ikulu Ndogo ya Zanzibar, tarehe 18 Agosti, 2026.






.jpeg)



.jpeg)






.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)
















.jpeg)

.jpeg)



.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)




