.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)

Jeshi la Polisi Wilaya ya Ngara, Mkoa wa Kagera, limeendelea kuwafikia wananchi na makundi mbalimbali yenye uhitaji katika jamii kwa lengo la kuimarisha ushirikiano na jamii, kutoa elimu pamoja na kuwajulia hali wananchi wanaolitegemea Jeshi hilo katika ulinzi wao na mali.
Katika mwendelezo wa shughuli hizo, Jeshi la Polisi Wilaya ya Ngara limetembelea na kutoa msaada wa vitu mbalimbali katika vituo vya kulelea watoto yatima Angel’s home pamoja na Kituo cha Kalkuta kilichopo Goyagoya, vinavyotoa huduma ya malezi kwa watoto yatima ambapo kituo hicho kina walea watoto kuanzia miaka 0 hadi 6.
Akiongoza maafisa, wakaguzi na askari wa vyeo mbalimbali, Mkuu wa Polisi Wilaya ya Ngara, Mrakibu wa Polisi (SP) Machumu Wang’uba amesema kuwa imekuwa ni utaratibu wa Jeshi la Polisi wilayani humo kuwafikia makundi yenye uhitaji kwa kuyapatia elimu mbalimbali pamoja na msaada wa mahitaji muhimu, ikiwa ni sehemu ya kuimarisha uhusiano kati ya Polisi na jamii.
Aidha, (SP) Wang’uba ameiomba jamii kuendelea kuyakumbuka na kuyasaidia makundi yenye uhitaji ili yajisikie kuwa sehemu ya jamii na kupata fursa sawa za kuishi kwa heshima kama makundi mengine katika Jamii.
Sambamba na hilo, ametoa wito kwa wananchi kuendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi kwa kutoa taarifa za vitendo vya ukatili na uhalifu vinavyotokea katika maeneo yao, ili hatua stahiki za kisheria ziweze kuchukuliwa dhidi ya wahusika.
Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dkt. Asha-Rose Migiro, amekutana na Wabunge wa Bunge la Jumuiya ya Afrika Mashariki (EALA) kutoka Tanzania Makao Makuu ya CCM, Dodoma, na kuwapongeza kwa dhamana ya kuiwakilisha nchi katika chombo hicho cha kikanda.
Katika mazungumzo hayo yaliyofanyika leo Julai 24,2026, Balozi Dkt. Asha-Rose Migiro,amewahimiza kuendelea kutanguliza maslahi ya Taifa na Jumuiya kwa kudumisha mshikamano, kujenga ushirikiano na wabunge kutoka nchi wanachama katika kuimarisha mtangamano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki ambao Tanzania inajivunia kuwa moja wa waasisi wake.
Katibu Mkuu amesisitiza kuwa Chama kina matarajio makubwa kwao na kitaendelea kuwapa ushirikiano wanapotekeleza wajibu wao wa kitaifa na kikanda.
MBUNGE wa Viti Maalum Mkoa wa Iringa, Nancy Nyalusi, amesema ujenzi wa jengo jipya la Mama na Mtoto ni hatua muhimu katika kuboresha huduma za afya na unatarajiwa kupunguza vifo vya wajawazito na watoto wachanga huku ukiimarisha upatikanaji wa huduma bora kwa wananchi wa Mkoa wa Iringa.
Nyalusi alitoa kauli hiyo wakati wa uzinduzi wa jengo hilo uliohudhuriwa na Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega, ambapo alimkaribisha wilayani Iringa na kueleza kuwa wananchi wa mkoa huo wanaendelea kushuhudia matokeo makubwa ya uwekezaji wa Serikali katika sekta mbalimbali za maendeleo.
Alisema Serikali imeendelea kuonyesha dhamira ya dhati ya kuboresha sekta ya afya kwa kujenga miundombinu ya kisasa inayowezesha wananchi kupata huduma bora karibu na maeneo yao.
"Jengo hili la Mama na Mtoto litasaidia kupunguza vifo vya akina mama na watoto wachanga, huku likiboresha mazingira ya utoaji wa huduma za afya hivyo tunamshukuru sana Rais na Serikali kwa kuendelea kutuletea miradi ya maendeleo inayogusa maisha ya wananchi," alisema Nyalusi.
Nyalusi alisema kuwa uwekezaji unaofanywa katika sekta ya afya umeongeza matumaini kwa wananchi, hasa wanawake na watoto ambao ndio wanufaika wakuu wa huduma hizo.
Pia aliwataka wananchi kutunza miundombinu hiyo ili iweze kuendelea kutoa huduma kwa ufanisi kwa miaka mingi ijayo.
Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Kheri James, alisema ujio wa Waziri wa Ujenzi ni fursa kwa Serikali kujionea hatua kubwa ambazo Mkoa wa Iringa umezipiga katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo.
Alisema uwepo wa Waziri huyo ni ishara ya namna Serikali ya Rais inavyofuatilia kwa karibu maendeleo ya miradi ya umma na kuhakikisha uwekezaji unaofanywa unaleta matokeo yaliyokusudiwa.
"Leo tumepata nafasi ya jicho la Mheshimiwa Rais kupitia Waziri wa Ujenzi mh Ulega kuona ni kwa kiwango gani tumepiga hatua kama wana Iringa," alisema Kheri.
James aliipongeza Halmashauri ya Manispaa ya Iringa kwa maandalizi mazuri ya hafla hiyo, akisema yameonyesha uwezo wa mkoa katika kupokea wageni wa kitaifa na kusimamia shughuli za maendeleo.
Aidha, aliisifu Hospitali ya Manispaa ya Iringa kwa ubora wa huduma zinazotolewa na watumishi wake, akieleza kuwa hospitali hiyo imekuwa mfano wa utoaji wa huduma zenye utu na kuwapa wagonjwa faraja tangu wanapowasili.
"Hii ni miongoni mwa hospitali zenye watumishi bora sana. Hapa tuna wahudumu wazuri ambao hata kabla hawajakupa dawa, maneno yao yanawafariji wagonjwa. Kuanzia mapokezi namna wananchi wanavyopokelewa, jambo hilo linatia moyo sana," alisema.
Kheri alisema mafanikio ya sekta ya afya hayategemei ujenzi wa majengo pekee bali pia yanahitaji watumishi wenye weledi, maadili na moyo wa kuwahudumia wananchi kwa upendo
Uzinduzi wa ujenzi wa jengo hilo la Mama na Mtoto unatajwa kuwa sehemu ya jitihada za Serikali za kuendelea kuboresha huduma za afya nchini kwa kujenga miundombinu ya kisasa,kuongeza ubora wa huduma na kupunguza vifo vinavyoweza kuzuilika kwa akina mama na watoto wachanga, huku wananchi wa Mkoa wa Iringa wakieleza matumaini makubwa kuwa huduma zitaboreshwa zaidi baada ya kuanza kutumika kwa jengo hilo.
Na Janeth Raphael - MichuziTv
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, amesema ikiwa angepewa nafasi ya kutoa ujumbe mmoja wa mwisho kwa Watanzania, basi usingekuwa mwingine zaidi ya kuwahimiza kuendelea kupambana kwa ajili ya kupata Katiba Mpya itakayokuwa na mwafaka wa kitaifa na kudumu kwa angalau miaka 50 ijayo.
Dkt. Nchimbi ametoa kauli hiyo leo jijini Dar es Salaam alipokuwa akizungumza katika Mkutano Mkuu wa Wanachama wa Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu, ambapo alizungumzia historia ya safari ya Tanzania kuelekea kupata Katiba Mpya na umuhimu wa kuendelea kujenga maridhiano katika mchakato huo.
Amesema mjadala kuhusu Katiba Mpya si wa leo wala wa jana, bali ni ajenda ambayo imeendelea kujadiliwa kwa zaidi ya miongo minne, huku akieleza kuwa vuguvugu la kuisukuma kwa nguvu lilianza mwaka 1992 baada ya kurejeshwa kwa mfumo wa vyama vingi vya siasa.
Kwa mujibu wa Makamu wa Rais, Tanzania imepitia hatua mbalimbali katika kutafuta Katiba Mpya, ikiwemo juhudi zilizofanywa na Serikali ya Awamu ya Nne iliyoanzisha rasmi mchakato wa kuandaa Katiba hiyo. Hata hivyo, alisema mchakato huo ulikumbana na changamoto mbalimbali kutokana na wingi wa maoni, matarajio na mahitaji yaliyowasilishwa na wananchi kutoka maeneo tofauti ya nchi.
Ameeleza kuwa Katiba ni msingi mkuu wa uongozi na maendeleo ya Taifa, hivyo inahitaji kujengwa kwa maridhiano mapana yatakayowakutanisha Watanzania wenye mitazamo tofauti kwa lengo la kuweka mbele maslahi ya Taifa badala ya maslahi binafsi au ya kisiasa.
Dkt. Nchimbi amesema mafanikio ya mchakato wa Katiba Mpya yatategemea uwezo wa Watanzania kuendelea kushiriki kwa uwazi, kuheshimiana na kujenga makubaliano yatakayozalisha Katiba imara, ya kisasa na inayokidhi mahitaji ya kizazi cha sasa pamoja na vizazi vijavyo.
"Kama nina kitu cha kuwaambia Watanzania, ningewaambia pambaneni mpate Katiba Mpya itakayodumu miaka 50, yenye mwafaka katika Taifa, itakayotupeleka mbele miaka 50," amesema Dkt. Nchimbi.
Ameongeza kuwa lengo la Katiba Mpya halipaswi kuwa kushinda au kushindwa kwa upande mmoja, bali kujenga msingi wa umoja, utulivu, haki na maendeleo endelevu ya Taifa kwa muda mrefu.
Kauli hiyo ya Makamu wa Rais imekuja wakati ambapo mjadala kuhusu mustakabali wa mchakato wa Katiba Mpya unaendelea kujitokeza katika maeneo mbalimbali nchini, huku wadau wa haki za binadamu, asasi za kiraia, viongozi wa dini, vyama vya siasa na makundi mengine ya kijamii wakiendelea kusisitiza umuhimu wa maridhiano na ushirikishwaji mpana wa wananchi katika kufikia Katiba inayokubalika na Watanzania wote.

Na Mwandishi Wetu
KAMPUNI ya Oryx Gas imekabidhi mitungi ya gesi ya kupikia 600 kwa makundi mbalimbali ya wajasiriamali wakimo mama lishe huku Mbunge wa Jimbo la Bagamoyo Subira Mgalu akieleza kuwa uamuzi wa Oryx kugawa mitungi hiyo kunakwenda kuondoa kabisa athari za kiafya zinazotokana na matumizi ya nishati chafu kama kuni na mkaa.
Mgalu ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge na Nishati na Madini ameyasema hayo leo Julai 24,2026 katika Tamasha la Samaki wilayani Bagamoyo ambapo kupitia tamasha hilo limetumika kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia ambapo yametolewa pia mafunzo ya matumizi salama ya nishati hiyo.
“Oryx Gas wamekuwa wadau wakubwa katika kuhamasisha nishati safi ya kupikia ya gesi ya LPG kwa vitendo na kupitia Samaki Festival wameamua kuunga mkono juhudi za Serikali kwa kugawa mitungi ya gesi kwa makundi mbalimbali yakiwemo ya Mama
Na Baba Lishe na wafanyabiashara wa soko la Samaki Bagamoyo.
“Tunafahamu kabla ya Serikali inayoongozwa na Rais Dk.Samia Suluhu Hassan ambaye ni kinara wa nishati Afrika kuja na kampeni ya nishati safi ya kupikia kulikuwa na matumizi makubwa ya kuni na mkaa hali iliyosababisha watumiaji wa nishati hiyo kuwa na athari za kiafya huku watu 32,000 wakipoteza maisha kutokana na madhara ya kutumia kuni na mkaa,”amesema Mgalu.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Oryx Energies Tanzania Imani Mtafya amesema katika kuunga mkono juhudi za Serikali kuhamasisha nishati safi ya kupikia wamekabidhi mitungi ya gesi 600 yenye thamani ya Sh.milioni 48 kwa makundi mbalimbali ya wajasiriamali.
Pia amesema kuanzia mwaka 2021 hadi mwaka 2026 wameshatoa mitungi 72000 yenye thamani ya Sh.bilioni 5.7 , lengo likiwa kuunga mkono juhudi za Serikali ambayo imeweka lengo ifikapo 2034 watumiaji wa nishati safi ya kupikia wawe wamefikia asilimia 80 kutoka asilimia 29 iliyopo sasa .
Mtafya amesema juhudi wanazofanya zinalenga pia kukomesha utumiaji wa kuni na mkaa ambao unaathiri kubwa sio tu kwa mazingira lakini kwa afya ya mtumiaji huku akifafanua kwasasa wanafanya uwekezaji mkubwa ili kuendana na sera ya Serikali ya kuhamasisha nishati safi ya kupikia.
“Tumewekeza katika ujenzi wa miundombinu ya ghala jipya la kuhifadhi gesi ambalo litagharimu Sh.bilioni 40 ili kuhakikisha tunaongeza usambazaji wetu wa gesi nchi nzima.”
Wakati huo huo Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo mkoani Pwani Shaibu Ndemanga aliyekuwa mgeni rasmi katika Tamasha la Samaki ametumia nafasi hiyo kuelezea mkakati wao katika kuhamasisha nishati safi ya kupikia na kwamba uamuzi wa Oryx Gas kugawa mitungi 600 ni hatua inayoonesha dhamira ya kuachana na kuni na mkaa hasa kwa wakaanga Samaki wa Soko la Bagamoyo .




.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)












.jpeg)




.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)









