Walimu nchini wametakiwa kuchukua jukumu kubwa katika kujenga kizazi chenye uelewa wa teknolojia na matumizi sahihi ya mifumo ya kidijitali ili kuiwezesha Tanzania kunufaika kikamilifu na uchumi wa kidijitali.

Hayo yamesemwa na Meneja wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) Kanda ya Kati, Mhandisi Asajile John, wakati wa mkutano na wadau wa elimu uliofanyika Mei 6, 2026 jijini Dodoma, amesema walimu wana nafasi muhimu katika kuhakikisha wanafunzi wanapata maarifa sahihi ya teknolojia tangu ngazi za awali.

Amesisitiza kuwa masomo ya sayansi, teknolojia, uhandisi na hisabati (STEM) ni msingi muhimu wa kujenga taifa lenye uwezo wa kushindana katika dunia ya kidijitali, aidha amezihimiza shule kuanzisha vilabu vya kidijitali vitakavyowawezesha wanafunzi kujifunza kwa vitendo, kujadiliana na kukuza ubunifu wao.

“Nadhani kama zilivyo Klabu za rushwa, hisabati n.k, nadhani ni wakati sasa wa shule kuanzisha vilabu vya kidijitali ili kuwajengea wanafunzi uelewa mpana wa teknolojia na kuwasaidia kuwa kuwajenga kuanzia ngazi ya awali”.

Akizungumzia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Mhandisi Asajile alibainisha kuwa inalenga kufikia angalau asilimia 70 ya Watanzania kuwa na uelewa wa matumizi ya teknolojia ya kidijitali, pamoja na kuhakikisha huduma nyingi zinaunganishwa katika mifumo ya kidijitali ili kuongeza tija.

Katika mkutano huo, pia aliwakumbusha wananchi kuwa makini na matumizi ya simu zao, akieleza kuwa katika kipindi cha miezi mitatu kuanzia Januari hadi Machi mwaka huu kumekuwepo na takribani majaribio ya uhalifu 9,800 kupitia ujumbe wa “tuma pesa kwa namba hii”.

Ameonya kuwa baadhi ya wahalifu hutumia laini zilizosajiliwa kwa majina ya watu wengine, hivyo wananchi wanapaswa kulinda laini zao kwani usajili wake ni mkataba wa kisheria unaohusisha namba ya NIDA na alama za vidole.

“Laini yako ni jukumu lako, Hakikisha haitumiki vibaya kwani unaweza kujikuta unaingia kwenye matatizo ya kisheria bila sababu,”.

Amehitimisha kwa kusema kuwa matumizi sahihi ya teknolojia ya mawasiliano yanaweza kurahisisha maisha, kuokoa muda na kuongeza ufanisi katika shughuli mbalimbali za maendeleo.




 

Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) umeboresha huduma zake kwa kuwarahisishia wanachama kujisajili, kupata taarifa na kufuatilia mafao yao kupitia simu za mkononi bila kulazimika kufika ofisini.

Akizungumza Mei 6, 2026 jijini Dodoma wakati wa mkutano wa wadau wa elimu wa mkoa huo, Meneja wa PSSSF Kanda ya Kati Lulyalya Sayi, amesema maboresho hayo yanalenga kumwezesha mchangiaji kukokotoa mafao yake na kufahamu jumla ya michango aliyowasilisha kwa urahisi zaidi.

Ameeleza kuwa mfuko huo ulianzishwa mwaka 2018 na unahudumia watumishi wa umma pamoja na sekta binafsi, kwa mujibu wa Sayi, PSSSF hutoa mafao ya aina mbili ambayo ni mafao ya muda mfupi na mafao ya muda mrefu.

Amesema Mafao ya muda mfupi yanawalenga wanachama wanaokumbwa na changamoto za muda, ikiwemo wanawake waliojifungua, wafanyakazi waliofukuzwa kazi, pamoja na wagonjwa,ambapo wanufaika hupatiwa mafao kuwasaidia kukabiliana na hali hizo.

Kwa upande wa mafao ya muda mrefu, amesema yanahusisha pensheni ya uzeeni kwa wanachama waliochangia kwa angalau miaka 15, na endapo mchangiaji atafariki baada ya kuanza kupokea pensheni, wategemezi wake watanufaika kwa kipindi cha miaka mitatu kupata mafao yake.

Aidha, mafao ya muda mrefu pia yanajumuisha, Mafao ya warithi, kwa wanachama waliotoa mchango kwa angalau miaka 15 lakini wakafariki kabla ya kustaafu wategemezi wao watapatiwa mafao hayo, lakini pia Mafao ya ulemavu, kwa wanachama wanaopata ulemavu kabla ya kufikia umri wa kustaafu, watapata mafao yao ili mradi wawe wamechangia kwa muda unaostahili.

Kwa sasa, wanachama wanaweza kutumia simu janja kuingia kwenye mfumo wa PSSSF (PSSSF Portal) kupitia google na kupata taarifa za michango  yao kwa urahisi badala ya kufika ofisini, amewataka wananchi kuendelea kujisajili na kufurahia huduma za mfuko huo.





Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB), Mhe. Balozi Meja Jenerali Mstaafu, Jacob Kingu ametoa wito kwa vikosi vya Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) vilivyopata miradi ya nishati safi ya kupikia kuwa mabalozi wa kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia kwa jamii zinazowazunguka.

Mwenyekiti Kingu ametoa wito huo leo Mei 5, 2026 wakati wa ziara ya Bodi hiyo iliyolenga kukagua utekelezaji wa miradi ya nishati safi ya kupikia inaayotekelezwa na Wakala wa Nishati Vijijini (REA) katika Kambi ya JKT ya Maramba mkoani Tanga.

Aidha, amesisitiza vijana wanaliopo kwenye kambi hizo za JKT kupatiwa mafunzo ya namna ya kutengeneza mkaa mbadala ili waweze kutumia ujuzi huo kujiajiri na kuwa mawakala wa kutengeneza mkaa mbadala pindi watakapomaliza mafunzo yao.

Kwa upande wake, akimwakilisha Mkuu wa JKT, Kanali Projest Rutaihwa aliishukuru menejimenti na Bodi ya REA kwa utekelezaji wa miradi nishati safi ya kupikia huku akiahidi kusimamia mradi huo unakuwa endelevu ili kuendelea kulinda mazingira pamoja na afya za wanaoandaa chakula.

Naye Luteni Kanali Thobias Ngailo, Meneja wa Nishati Safi ya Kupikia kutoka JKT, ameeleza kuwa jumla ya vikosi 22 vimenufaika na fedha zilizotolewa na Serikali kupitia REA ambapo amesema mashine 30 kati ya 60 za kutengeneza mkaa mbadala zimeshasambazwa katika vikosi na zinaendelea kufanya kazi, hatua inayotarajiwa kuongeza uzalishaji na matumizi ya nishati safi kwa kiwango kikubwa. 











Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amewasili katika Kanisa la Anglikana Dayosisi ya Ruvuma kushiriki Ibada ya Mazishi ya aliyekuwa Askofu wa Pili wa Anglikana Dayosisi ya Ruvuma na Katibu Mkuu Mstaafu wa Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT) Marehemu Askofu Stanford Shauri, Ibada inayofanyika Liuli Wilaya ya Nyasa mkoani Ruvuma leo tarehe 06 Mei 2026.



Na Mwandishi Wetu.

CHAMA cha Wafanyakazi wa Wakusanya Mapato Tanzania (TAREWU) kimesaini Hati ya Makubaliano (MoU) na Taasisi ya Usimamizi wa Vihatarishi Tanzania (IRMT) kwa lengo la kuimarisha ushirikiano katika maendeleo ya kitaaluma na mafunzo ya usimamizi wa vihatarishi.

Makubaliano hayo yamesainiwa jijini Dar es Salaam, yakilenga kuwajengea uwezo wanachama wa TAREWU ili kuongeza ufanisi na tija katika sekta ya ukusanyaji mapato nchini.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mwenyekiti wa IRMT, CPA Pius Maneno, amesema taasisi yake ipo tayari kutoa mafunzo yenye viwango vya kimataifa na kushirikiana katika kukuza taaluma ya usimamizi wa vihatarishi.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa TAREWU, Lutufyo Mtafya, amesema makubaliano hayo ni hatua muhimu katika utekelezaji wa mpango mkakati wa chama hicho unaolenga kuwafanya wanachama wake kuwa na ujuzi shindani unaoendana na mabadiliko ya kiuchumi duniani.

Amesema kupitia ushirikiano huo, wanachama watanufaika na programu za mafunzo, ushauri wa kitaalamu pamoja na fursa za kukuza ujuzi katika maeneo ya kisasa ya usimamizi wa vihatarishi.

Naye Katibu wa IRMT, Christopher Njovu, amesema ushirikiano huo utasaidia kuongeza uelewa wa masuala ya vihatarishi katika sekta ya ukusanyaji mapato na kusisitiza umuhimu wa taaluma hiyo katika kulinda rasilimali za taasisi.

Kwa upande wa TAREWU, Katibu wake, Wakili Michael Marere, amesema makubaliano hayo yatakuwa chachu ya maendeleo endelevu kwa wanachama na sekta nzima ya mapato nchini.

TAREWU imeeleza kuwa ina imani ushirikiano huo utafungua ukurasa mpya wa mafanikio, huku IRMT ikiahidi kuendelea kushirikiana kwa karibu kuhakikisha malengo yaliyokusudiwa yanafikiwa.



Na Mwandishi wetu

MKUU wa Mkoa wa Geita, Martin Shigela anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika maadhimisho ya Siku ya Punda Duniani yatakayofanyika kitaifa Mei 8, 2026 katika Kijiji cha Mgusu, Manispaa ya Geita.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Wizara ya Mifugo na Uvuvi, maandalizi ya tukio hilo yamekamilika, huku shughuli za awali zikitarajiwa kuanza Mei 6 hadi 7 kwa kutoa huduma za matibabu kwa punda pamoja na elimu kwa wafugaji na jamii.

Taarifa hiyo imeeleza kuwa kipindi hicho, kliniki maalumu zitahudumia takribani punda 700 katika maeneo ya Mgusu, Magenge na mji wa Geita. Sambamba na hilo, elimu kuhusu utunzaji bora, lishe na matumizi sahihi ya vifaa vya punda itatolewa ili kuboresha ustawi wa wanyama hao.

"Zaidi ya wanafunzi 3,800 pamoja na wanajamii watanufaika na programu za elimu zitakazowasilishwa kupitia maonesho ya vitendo, sanaa na kampeni za uhamasishaji, lengo likiwa ni kujenga kizazi chenye uelewa wa kulinda rasilimali hiyo muhimu,"ilieleze taarifa hiyo.

Maadhimisho hayo yatakuwa jukwaa muhimu la kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa ustawi wa punda, yakiongozwa na kaulimbiu isemayo, “Kulinda Punda wa Afrika ni Wajibu Wetu Sote.” Kaulimbiu hiyo inalenga kuibua uelewa mpana juu ya changamoto zinazowakabili punda na haja ya kuchukua hatua za pamoja kuwalinda.

Rais wa Kenya, Mhe. Dkt. William Ruto, ameusifu uwekezaji wa Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) wa Tanzania unaoendelea jijini Nairobi, akisema ni mfano bora wa matumizi sahihi ya akiba za wanachama katika kukuza uchumi na maendeleo ya kikanda.

Akizungumza Mei 5, 2026 wakati akihutubia Bunge jijini Dodoma, Mhe. Dkt. Ruto alimpongeza Mkurugenzi Mkuu wa NSSF Tanzania, Bw. Masha Mshomba, kwa usimamizi thabiti wa uwekezaji huo, akibainisha kuwa unaonesha namna bora ya kugeuza akiba za wanachama kuwa miradi yenye tija.

Alisema mradi huo uliopo eneo la Upper Hill, jijini Nairobi, unahusisha ujenzi wa majengo pacha yenye ghorofa 22, unaogharimu takribani dola za Marekani zaidi ya Milioni 51. Mradi huo unatekelezwa kwa kutumia akiba za wanachama wa NSSF Tanzania na unatarajiwa kukamilika ndani ya kipindi cha miaka miwili.

Mhe. Dkt. Ruto alieleza kuwa uwekezaji huo ni somo muhimu kwa Kenya na mataifa mengine ya Afrika Mashariki kuhusu umuhimu wa kukuza utamaduni wa akiba na uwekezaji kwa maendeleo ya muda mrefu.

“Uwekezaji ni zao la akiba. Huwezi kuwekeza kama huna akiba,” alisisitiza Dkt. Ruto, akihimiza wananchi na taasisi kuzingatia nidhamu ya kuchangia katika mifuko ya hifadhi ya jamii kwa mustakabali wa baadaye.

Aidha, alibainisha kuwa nchini Kenya wamefanya maboresho ya mfumo wa hifadhi ya jamii mwaka 2023 baada ya kujifunza kutoka mifumo bora ikiwemo ya Tanzania.

Alieleza kuwa mfumo huo unahitaji mwajiri na mwajiriwa kuchangia kwa pamoja hadi asilimia 20 ya mapato ili kuimarisha usalama wa kifedha kwa wafanyakazi wanapostaafu.

Mhe. Dkt. Ruto alisisitiza kuwa utamaduni wa kujiwekea akiba unapaswa kuendelezwa ndani ya jamii, akieleza kuwa hatua hiyo ni muhimu katika kujenga mifumo imara ya hifadhi ya jamii.

Rais Dkt. Ruto pia alisifu mafanikio ya Tanzania katika sekta ya hifadhi ya jamii, akieleza kuwa Kenya inaendelea kujifunza na kuchukua mifano bora kutoka kwa majirani zake.

Katika kuimarisha ushirikiano wa kikanda, alisema anajivunia uhusiano mzuri uliopo kati ya Kenya na Tanzania chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, akibainisha kuwa huu ni wakati muhimu katika historia ya mataifa hayo mawili.

Akihitimisha, Dkt. Ruto amesema kuwa kwa sasa kuna hatua kubwa ya kihistoria katika uhusiano wa Kenya na Tanzania, akieleza furaha yake kwa ushirikiano wa karibu kati yake na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Amesema viongozi hao wanafanya kazi kwa pamoja kuwaleta karibu wananchi wa Afrika Mashariki na kuondoa changamoto zilizodumaza maendeleo kwa muda mrefu.

Kauli hiyo inaakisi mwelekeo wa mataifa ya Afrika Mashariki katika kutumia rasilimali zao za ndani kama kichocheo cha ukuaji wa uchumi na ustawi wa wananchi.

Rais Dkt. William Ruto anahitimisha ziara rasmi ya siku mbili nchini Tanzania, iliyoanza Mei 4 hadi 5, 2026.






















Na MWANDISHI WETU

MKUU wa Wilaya ya Kisarawe, Petro Magoti, ametangaza operesheni kali dhidi ya wanaojihusisha na uvujaji wa mapato wilayani humo na kumwagiza Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya hiyo, Aidan Kitare, kuivunja Kikosi Kazi cha Mapato (KKM) kinacho husika na usimamizi wa mapato.

Aidha ametoa onya kali kwa baadhi ya madiwani watakao jaribu kulalamika baada ya kuondolewa au jamaa zao kuondolewa katika kamati hiyo kutokana na kubainika kushiriki katika kuhujumu mapato.Magoti, aliyasema hayo alipohutubia kikao cha Baraza la Madiwani la Wilaya ya Kisarawe, mkoani Pwani.

Ameeleza kusikitishwa na uvujaji mkubwa wa mapato katika wilaya hiyo hali inayo kwamisha maendeleo."Watu wana kula kwelikweli. Wanakula vibaya mno halafu wanalalamika. Nataka niwaambie tumefahamiana kwa sababu ya kazi, tofauti na kazi sina udugu nanyie. Tufanye kazi , tumsaidie Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, kutekeleza majukumu,"amesema Magoti.

Amesema, dhamira ni kujenga Kisarawe inayo heshimu mali na mapato ya serikali ambapo kama mianya ya uvujaji wa mapato itadhibitiwa wilaya hiyo inaweza kukusanya sh.bilioni 7 tofauti na sh. bilioni 4 inazo kusanya sasa.
"Unakwenda sehemu unakuta waliumu wana kaa chini. Hawana ofisi. Hii ni aibu. Mapato yanaliwa na watu wachache,"amebainisha Magoti.

Amesema ana faili maalumu la wahusika wanao jihusisha kuhujumu mapato pamoja na maeneo yote yanayo tumika."Ninafaili hili hapa. Wahusika wote wanaohujumu mapato. Diwani ukiwa na malalamiko yoyote fika ofisini kwa Mwenyekiti wa Halmashauri au kwa mkurugenzi akulete kwa mkuu wa wilaya na ukibainika unahusika au ndugu yako unaye mtetea anahusika tukakupa ushahidi tutakuchukulia hatua,"amedai Magoti.

Amesema anataarifa za kila mtu aliyeondolewa katika Kikosi Kazi cha Mapato ya halmashauri hiyo kupitia faili maalumu la wahujumu wa mapato.

"Diwani yoyote anaye jua kwamba ndugu yake alikula mapato taarifa zake ninazo humu katika falili.Diwani yoyote atakaye piga kelele nitamkamata,"ameonya Magoti.
Ameeleza, diwani kuwa na ndugu anaye kusanya mapato siyo dhabi bali dhambi ni kumtumia ndugu yake huyo kujipatia mapato na kuibia halmashauri.

"Kwa Mamlaka niliyo nayo ninakuelekeza mkurugenzi kuvunja kikosi hicho hadi kufikia pia ukae na Kamati ya Usalama ya wilaya kuunda kikosi kipya,"amesema
Magoto amesema kikosi hicho kikundwa kikiundwa, kipewe semina na kiingie kazini kutekeleza majukumu ya kukusanya mapato.

Aliongeza; "Na hiki mkurugenzi ndiyo kipimo chako cha kwanza cha kujua unatosha ama utoshoshi. Mimi ndiyo nina vyombo. Hakuna mtu yoyote mwenye vyombo katika wilaya hii. Mkurugenzi usiogope. Mimi ndiyo naweza kusema uwepo au usiwepo kwa hiyo fanya kazi,".

Aidha ameelekeza polisi wilayani humo kumsakama mmiliki mmoja wa jengo la ghorofa jirani na ofisi za halmashauri hiyo ambalo alisema lina husika katika vitendo vya kuhujumu mapato.

"Kuna kijengo cha ghorofa jirani na hapa halmashauri. Mwiteni mmiliki anieleze shughuli zinazofanyika pale hadi saa saba usiku na kuanza kesho usiku (leo) wote watao kuwa pale wakamatwe,"amesema.Ameeleza mmiliki wa jengo hilo ambaye ni mwanamke afikishwe mbele yake kabla ya saa 9:00 alasili jana kujieleza.

Katika hatua nyingine, Magoti alitangaza kufanya operesheni ya kuvunja nyumba zilizojengwa kinyume cha sheria katika eneo la serikali la Homboza na kwamba katika operesheni hiyo aliyo ibatiza jina la Kanyamazongo atawatia mbaloni mabalozi saba wanaopinga jitihada za serikali.

"Hatuhitaji watu wanao hujumu serikali.Pale halmashauri itaingiza shilingi bilioni 5.8. Kuna shule imejengwa pale halmashauri ili nunua eneo lake yenyewe.Ni vitu vya ajabu sana,"amesema .

Aidha Magoti alitaja vizuizi vinavyoongoza kwa kuiba mapato wilayani humo na kuyatorosha kuwa ni Homboza, Kwa Pinda, Kiluvya Kisokwa, Ikuruwi, Kauzeni, Msanga na Masaki.

" Kuna watu wanachukua fedha taslimu pale.Tunaorodha yao humu katika faili. Tutakamata baiskeli, pikipi, magari na kila muhusika,"ameeleza Magoti.
Kuhusu watu wanaouza kiholela maeneo hususan katika eneo la Cha Kenge, Magoti amesema Operesheni Kanyazongo itamkumba kila muhusika.

"Madiwani niwaombe nyie ndiyo viongozi wa kamati za maendeleo za kata kwa hiyo kama eneo lako linauza viwanja kinyume cha utaratibu tutakuhoji,"amesema


















Mkuu wa Wilaya ya Moshi, Mhe. Godfrey Eliakimu Mnzava, akiwa ameambatana na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya, viongozi wa siasa, pamoja na timu ya wataalamu wa Halmashauri ya Wilaya ya Moshi, amefanya ziara ya kikazi kutembelea na kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo iliyopendekezwa kupitiwa na Mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka 2026.

Katika ziara hiyo, Mhe. Mnzava alikagua mradi wa Kituo cha Mafuta cha Mavoa kilichopo Kitongoji cha Njiapanda Magharibi, Kata ya Njiapanda, pamoja na mradi wa Zahanati ya Ghona uliopo Kijiji cha Ghona katika Kata ya Kahe Mashariki. 

Aidha, Mkuu wa Wilaya na timu yake walifika katika Shule ya Sekondari Mwika ambapo ndipo litakapokuwa eneo la mapokezi ya Mbio za Mwenge wa Uhuru 2026, eneo ambalo pia Mwenge utajionea programu maalum ya matumizi ya Nishati Safi.

Miradi mingine iliyofanyiwa ukaguzi ni pamoja na ujenzi wa barabara katika Kata ya Kilema Kusini, mradi wa maji wa Kijiji cha Mabungo uliopo Kata ya Kirua Vunjo Kusini, pamoja na mradi wa vijana na uzalishaji wa madini ya ujenzi. 

Vilevile, ziara hiyo ilihusisha ukaguzi wa ujenzi wa Ofisi ya Kata ya Kimochi na ujenzi wa Shule ya Amali ya Sekondari Chemchem iliyoko Manushi katika Kata ya Kibosho Magharibi.

Mbio za Mwenge wa Uhuru kwa mwaka 2026 zinatarajiwa kuingia mkoani Kilimanjaro tarehe 28 Juni 2026 na kukimbizwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Moshi ifikapo tarehe 01 Julai 2026. 

Mwenge huo utaongozwa na kaulimbiu isemayo: “Tanzania ni Yetu Sote, Tushikamane kwa Pamoja Kuleta Maendeleo.









Kaimu Mkurugenzi wa Manispaa ya Kahama, Stephen Magalla, akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo kwa watoa huduma za afya yaliyoandaliwa kwa lengo la kuimarisha mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia (GBV) na ukatili dhidi ya watoto (VAC) katika Halmashauri ya Manispaa ya Kahama, mkoani Shinyanga.


Kaimu Mkurugenzi wa Manispaa ya Kahama, Stephen Magalla, akifungua mafunzo ya kuimarisha mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia (GBV) na ukatili dhidi ya watoto (VAC) kwa watoa huduma za afya katika Halmashauri ya Manispaa ya Kahama, Shinyanga.

**Shirika la Tanzania Health Promotion Support (THPS), kwa kushirikiana na Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali (GCLA) na kwa ufadhili wa Sanlam Allianz, limeanza rasmi kuendesha mafunzo ya kuimarisha mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia (GBV) na ukatili dhidi ya watoto (VAC) katika Halmashauri ya Manispaa ya Kahama, mkoani Shinyanga.

Mafunzo haya yanatekelezwa kupitia Mradi wa Paza Sauti+ unaolenga kuiwezesha jamii kuzungumza wazi dhidi ya ukatili huku ukijenga uwezo wa watoa huduma za afya katika ukusanyaji na matumizi sahihi ya ushahidi wa kiforensiki.

Mradi wa Paza Sauti+ unalenga kuimarisha uwezo wa kiforensiki kwa uchunguzi unaotegemea ushahidi, kuhamasisha kutoa taarifa za matukio kwa wakati na kwa usalama, kuongeza uelewa wa umuhimu wa ushahidi wa vinasaba (DNA) katika upatikanaji wa haki na kuimarisha uratibu kati ya sekta za afya, polisi na ustawi wa jamii.

Mafunzo kwa watoa huduma wa afya yanafanyika kuanzia tarehe 5 hadi 7 Mei 2026, yakifuatiwa na mafunzo maalum kwa Wahudumu wa Afya ya Jamii (CHWs) tarehe 8 Mei 2026.

Lengo ni kuimarisha mifumo ya utambuzi wa mapema, uripoti wa matukio, ukusanyaji wa ushahidi na utoaji wa huduma bora kwa manusura.

Kupitia mafunzo haya, washiriki wanapatiwa ujuzi wa kutambua matukio ya ukatili mapema, Kuripoti kwa wakati na kwa usahihi, kukusanya na kuhifadhi ushahidi wa kiforensiki ipasavyo na kutoa huduma zinazomlenga manusura

Akizindua rasmi mafunzo hayo, Kaimu Mkurugenzi wa Manispaa ya Kahama, Stephen Magalla, amepongeza ushirikiano kati ya THPS, GCLA na Sanlam Allianz.

“Ushirikiano huu unaakisi mwitikio shirikishi unaohitajika katika kukabiliana na ukatili wa kijinsia na ukatili dhidi ya watoto. Kuimarisha mifumo ya kiforensiki na uwezo wa watoa huduma kutaboresha kwa kiasi kikubwa msaada kwa manusura na kuhakikisha wanapata haki kwa wakati,” amesema Magalla.

Kwa upande wake, Ndugu Julius Magabe, Mtendaji Mkuu wa Sanlam Allianz Life Insurance Tanzania, alisisitiza dhamira ya kampuni hiyo katika kuunga mkono mradi wa Paza Sauti+.

“Tunajivunia kuwa sehemu ya mradi huu muhimu. Tumeamua kuunga mkono Mradi wa Paza Sauti+ kama mchango wetu katika kupunguza na kupambana na ukatili wa kijinsia na ukatili dhidi ya watoto. Kama taasisi inayolinda maisha kupitia huduma za bima, tunatambua umuhimu wa kuunga mkono juhudi zinazolinda ustawi na heshima ya jamii.”

Washiriki wa mafunzo ni pamoja na watoa huduma za afya, maafisa wa dawati la jinsia kutoka Jeshi la Polisi, maafisa ustawi wa jamii na wadau wa kijamii.

Mafunzo haya yanawawezesha kuimarisha mchango wao katika mnyororo mzima wa kushughulikia masuala ya ukatili wa kijinsia na ukatili dhidi ya watoto, kuanzia utambuzi wa mapema hadi usimamizi wa kesi.

Uzinduzi huo umehudhuriwa na viongozi wa serikali wa ngazi ya mkoa, ukiashiria dhamira thabiti ya kisiasa na taasisi katika kukabiliana na vitendo vya ukatili na kuboresha upatikanaji wa haki kwa manusura.

Aidha, katika hafla hiyo walikuwepo pia Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (OC-CID) Kahama, SP Maro Kenyunko, pamoja na Afisa Ustawi wa Jamii wa Halmashauri ya Mji wa Kahama, Abrahamani Kibakaya, ambao wameipongeza THPS, GCLA na Sanlam Allianz kwa hatua za wakati muafaka katika kuziba mapengo yaliyopo kwenye kushughulikia masuala ya ukatili wa kijinsia na ukatili dhidi ya watoto kupitia Mradi wa Paza Sauti+.

Wadau wamebainisha changamoto zinazoendelea katika ukusanyaji na matumizi ya ushahidi wa kiforensiki, hali inayochangia kuchelewesha au kudhoofisha mashauri ya ukatili wa kijinsia na ukatili dhidi ya watoto.

Mradi huu unalenga kuziba mapengo hayo kwa kujenga uwezo wa kitaalamu na kuongeza uelewa wa jamii juu ya umuhimu wa kuripoti mapema.

Mradi wa Paza Sauti+ unatekelezwa katika Hospitali ya Wilaya ya Kahama na Kituo cha Afya Nyasubi, ukihusisha kata za Nyasubi na Malunga, ukiendana na Mpango wa Kitaifa wa Kutokomeza Ukatili dhidi ya Wanawake na Watoto (NPA-VAWC II).

Kwa kuimarisha mifumo na ushiriki wa jamii, Mradi wa Paza Sauti+ unalenga kuhakikisha manusura wanasikilizwa, wanapatiwa huduma bora kwa wakati, na wanapata haki stahiki.

THPS pia inaipongeza Sanlam Allianz kwa mchango wake katika kupambana na ukatili kupitia programu za uwajibikaji kwa jamii.


Kuhusu THPS


Tanzania Health Promotion Support (THPS) ni shirika lisilo la kiserikali lililosajiliwa nchini, linalojikita katika kuboresha upatikanaji wa huduma bora za afya na ustawi wa jamii kwa Watanzania wote. Tangu mwaka 2011, THPS imekuwa ikishirikiana na Serikali ya Tanzania kuimarisha mifumo ya afya na jamii kupitia mbinu mbalimbali zinazotegemea Ushahidi wa kisayansi.


Kuhusu Paza Sauti+


Mradi wa Paza Sauti+ ni mpango unaoshirikisha Serikali na sekta binafsi unaolenga kuimarisha sauti za jamii, kujenga uwezo wa taasisi, na kuboresha upatikanaji wa haki kwa manusura wa ukatili wa kijinsia na ukatili dhidi ya watoto nchini Tanzania.

Kaimu Mkurugenzi wa Manispaa ya Kahama, Stephen Magalla, akifungua mafunzo ya kuimarisha mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia (GBV) na ukatili dhidi ya watoto (VAC) kwa watoa huduma za afya katika Halmashauri ya Manispaa ya Kahama, Shinyanga.

Kaimu Mkurugenzi wa Manispaa ya Kahama, Stephen Magalla, akifungua mafunzo ya kuimarisha mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia (GBV) na ukatili dhidi ya watoto (VAC) kwa watoa huduma za afya katika Halmashauri ya Manispaa ya Kahama, Shinyanga.

Mganga Mkuu Halmashauri ya Manispaa ya Kahama, Dkt. Baraka Msumi akizungumza kwenye mafunzo ya kuimarisha mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia (GBV) na ukatili dhidi ya watoto (VAC) kwa watoa huduma za afya katika Halmashauri ya Manispaa ya Kahama, Shinyanga.

Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (OC-CID) Kahama, SP Maro Kenyunko akizungumza kwenye mafunzo ya kuimarisha mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia (GBV) na ukatili dhidi ya watoto (VAC) kwa watoa huduma za afya katika Halmashauri ya Manispaa ya Kahama, Shinyanga.

Afisa Sheria kutoka Ofisi ya Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali, Mohamed Mdemu akizungumza kwenye mafunzo ya kuimarisha mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia (GBV) na ukatili dhidi ya watoto (VAC) kwa watoa huduma za afya katika Halmashauri ya Manispaa ya Kahama, Shinyanga.

Mratibu wa Mradi wa Paza Sauti + kutoka Shirika la Tanzania Health Promotion Support (THPS), Agnes Kirato akielezea mradi wa Paza Sauti +

Mratibu wa Mradi wa Paza Sauti + kutoka Shirika la Tanzania Health Promotion Support (THPS), Agnes Kirato akielezea mradi wa Paza Sauti +

Mratibu wa Mradi wa Paza Sauti + kutoka Shirika la Tanzania Health Promotion Support (THPS), Agnes Kirato akielezea mradi wa Paza Sauti +












Top News