
Serikali itaendelea kushirikiana kwa karibu na wawekezaji wa sekta ya viwanda ili kutatua changamoto zinazokwamisha uzalishaji na kuweka mazingira bora yatakayochochea ukuaji wa uchumi wa viwanda nchini.
Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe.Judith Kapinga mara baada ya kufanya ziara katika kiwanda kikubwa cha kuchakata na kuzalisha mafuta ya kula cha Mainland Group Agro Process Tanzania jijini Dodoma, ambapo amejionea shughuli mbalimbali za uzalishaji na kiwango cha uwekezaji kilichofanyika katika kiwanda hicho.
Akizungumza baada ya kutembelea mitambo ya uzalishaji, Waziri Kapinga amesema Serikali inatambua mchango mkubwa wa sekta binafsi katika kukuza uchumi, kuongeza ajira na kuimarisha mapato ya Taifa, hivyo itaendelea kuhakikisha changamoto zinazowakabili wawekezaji zinapatiwa ufumbuzi kwa wakati.
Amesema ameoneshwa kuvutiwa na uwekezaji mkubwa uliofanyika katika kiwanda hicho na kusisitiza kuwa viwanda vya kuongeza thamani ya mazao ya ndani vina nafasi muhimu katika kufanikisha malengo ya maendeleo ya Taifa pamoja na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
“Tunataka kuona mazao yanayozalishwa na wakulima wetu yanaongezewa thamani hapa hapa nchini. Hii ndiyo njia sahihi ya kuongeza tija kwa mkulima, mfanyabiashara, mwekezaji na Serikali kwa ujumla,” amesema Kapinga
Amebainisha kuwa licha ya Tanzania kuwa miongoni mwa wazalishaji wakubwa wa mazao ya mafuta, bado uzalishaji wa mafuta ya kula haujakidhi mahitaji ya ndani, hali inayolazimu nchi kuagiza sehemu ya mafuta kutoka nje.
Kutokana na hali hiyo, amesema Serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali ikiwemo maboresho ya sera, sheria na mifumo ya kodi ili kuvutia uwekezaji zaidi katika viwanda vya mafuta ya kula na kuongeza uzalishaji wa ndani.
Waziri huyo amesema Serikali inalenga kuona nchi inafikia kujitosheleza kwa mafuta ya kula katika miaka ijayo kwa kuongeza uzalishaji wa malighafi na kuimarisha uwezo wa viwanda vilivyopo.
Katika mazungumzo yake na viongozi wa kiwanda hicho, ameelezwa kuwa changamoto kubwa inayokikabili ni upatikanaji mdogo wa malighafi, hususan mbegu za mazao ya mafuta, jambo linalofanya kiwanda kufanya kazi chini ya uwezo wake licha ya uwekezaji mkubwa uliowekwa.
Aidha, Serikali imeanza kushirikiana na Wizara ya Kilimo pamoja na taasisi zake kuweka mikakati ya kuongeza uzalishaji wa mazao ya mafuta ili kuhakikisha viwanda vinapata malighafi za kutosha na kutumia uwezo wake kikamilifu.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa kiwanda hicho, Bw. Jiaweli Chen, ameipongeza Serikali ya Tanzania kwa kuendelea kuboresha mazingira ya uwekezaji na kutoa ushirikiano unaowezesha viwanda kufanya kazi kwa ufanisi na kuchangia maendeleo ya uchumi wa nchi.
Amesema kuwa sera na hatua mbalimbali zinazochukuliwa na Serikali zimeongeza imani kwa wawekezaji, jambo ambalo limechangia ukuaji wa shughuli za uzalishaji na kuongeza ajira kwa wananchi katika maeneo mbalimbali nchini.
Bw. Chen pia ameishukuru Serikali kwa kutembelea mradi huo na kusikiliza changamoto zinazowakabili, akieleza kuwa hatua hiyo inaonesha utayari wa viongozi kushirikiana na sekta binafsi katika kutafuta suluhisho la changamoto zinazojitokeza wakati wa utekelezaji wa shughuli za uzalishaji.
Hatahivyo amesema kuwa kiwanda hicho kitaendelea kushirikiana na Serikali katika kuongeza uzalishaji, kuimarisha ubora wa bidhaa na kuchangia jitihada za taifa za kukuza sekta ya viwanda, huku akieleza matumaini yake kuwa changamoto zilizowasilishwa zitapatiwa ufumbuzi kwa manufaa ya wawekezaji na wananchi kwa ujumla.




.jpeg)
.jpeg)







.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)


.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)









.jpeg)
.jpeg)
