Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, akiwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa N’djili, Kinshasa, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo leo tarehe 14 Novemba 2025. Makamu wa anamwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika Mkutano wa Tisa wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Jumuiya ya Nchi za Maziwa Makuu utaofanyiika Jijini Kinshasa tarehe 15 Novemba 2025.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, akipokelewa na Waziri wa Biashara za Kimataifa wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo Mhe. Julien Paluku Kahongya, wakati akiwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa N’djili, uliyopo Jijini Kinshasa, leo tarehe 14 Novemba 2025. Makamu wa anamwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika Mkutano wa Tisa wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Jumuiya ya Nchi za Maziwa Makuu utaofanyiika Jijini Kinshasa tarehe 15 Novemba 2025.


Na Mwandishi wetu- Dodoma
RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema Serikali itaendelea kukuza Sekta ya Utalii ikilenga kufikia watalii wa ndani na wa nje milioni nane (8) ifikapo mwaka 2030.

Ameyasema hayo alipokuwa analihutubia na kufungua Bunge la 13 la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania leo tarehe 14, Novemba, 2025, Bungeni jijini Dodoma.

“Kutokana na wingi na ubora wa vivutio vya utalii pamoja utamaduni mkubwa wa kiutamaduni Tanzania tunaweza kufikia lengo hili na tutafungamanisha vivutio vya utalii ili mtalii atumie siku nyingi zaidi akiwa nchini Tanzania.” amesisitiza Rais Samia na kusema sekta hiyo ina mchango mkubwa sana kwenye Uchumi.

Aidha, Rais samia ameahidi kuboresha vyuo vya utalii na ukarimu kwa kuongeza idadi ya watoa huduma wenye weledi katika fani zote kwenye sekta hiyo ya utalii na ukarimu.

‘Sekta hii nayo ni sehemu muhimu ya kuzalisha ajira kwa wananchi na kutuongezea akiba ya fedha za kigeni’ amesema Rais Samia.

Pia, Rais Samia amefafanua kuwa Serikali itaendeleza jitihada za uhifadhi na utunzaji wa maliasili sambamba na kupambana na ujangili.

“Hatuna budi kuongeza nguvu kukabiliana na changamoto ya wanyama waharibifu inayokabili jamii mbalimbali zinazopakana na hifadhi kote nchini’ amesema Rais Samia.

Rais Samia amesema pia Serikali itaongeza askari ,vituo vya ulinzi,mbinu na vifaa vya kisasa ikwemo ndegenyuki kwa kukabiliana na janga la wanyama waharibifu.


Na Saidi Lufune, Dodoma
WIZARA ya Maliasili na Utalii inaendelea kushirikiana na wadau wa sekta ya misitu na ufugaji nyuki ili kuboresha uhifadhi na uendelezaji wa rasilimali za misitu na nyuki, pamoja na kukabiliana na changamoto zinazokabili sekta hizi. Lengo ni kuhakikisha faida za sekta hizi zinanufaisha jamii na taifa kwa ujumla.

Hayo yalielezwa jijini Dodoma na Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Misitu na Nyuki wa Wizara hiyo, Bw. Daniel C. Pancras, wakati wa ufunguzi wa warsha iliyowakutanisha wataalamu na wadau wa sekta ya misitu na nyuki. Warsha hiyo ililenga kujenga uelewa wa pamoja kuhusu mikakati ya kuendeleza sekta hizi na kuongeza ufanisi katika usimamizi wa rasilimali za misitu na nyuki.

“Sekta ya misitu na nyuki imekuwa na mchango mkubwa katika ongezeko la ajira kwa vijana na wanawake, na pia imechangia kwa kiasi kikubwa katika ukuaji wa uchumi wa taifa. Hata hivyo, sekta hii inakabiliwa na changamoto kadhaa, na kupitia warsha hii, tunapanga mikakati ya pamoja ya kutatua changamoto hizo,” alisema Bw. Pancras.

Akiendelea, Pancras alisisitiza kuwa mikakati inayopendekezwa katika warsha hii inapaswa kutoa matokeo chanya na ya haraka katika utekelezaji wa sera na malengo ya Wizara, huku ikizingatia Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050. Hii ni pamoja na kuendeleza viwanda vya kuongeza thamani ya mazao ya misitu na asali, na kuhakikisha sekta ya misitu inapata maendeleo endelevu.

Katika hatua nyingine, Pancras alitoa wito kwa wadau wa sekta ya uhifadhi na utalii kushiriki kikamilifu katika kuwania Tuzo za Uhifadhi na Utalii, maarufu kama The Serengeti Awards. Tuzo hizi zinatolewa kwa kutambua michango ya wadau katika kuendeleza sekta ya maliasili na utalii nchini. Alisisitiza umuhimu wa wadau kuwa mabalozi wazuri kwa kuhamasisha wengine kuhusu uwepo wa tuzo hizi.

Wadau walioshiriki warsha hiyo ni pamoja na Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, Wizara ya Viwanda na Biashara, Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Mfuko wa Misitu Tanzania (TaFF), vyuo vilivyo chini ya Wizara ya Maliasili na Utalii, Tanzania Beekeepers Development Organization (TABEDO), wawakilishi kutoka Ofisi za Wakuu wa Mikoa ya Dodoma na Morogoro, Shirika la Nyumba la Taifa, na Bodi ya Wandalasi.








Watumishi wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA) wamepongezwa kwa kujituma na kufanya kazi kwa bidii hali iliyopelekea mafanikio makubwa ya Wakala huo ikiwamo kufikisha umeme katika Vijiji vyote vya Tanzania Bara.

 Pongezi hizo zimetolewa leo Novemba 14, 2025 na Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali watu kutoka Wizara ya Nishati, Bi. Ziana Mlawa wakati wa Kikao cha Pili cha Baraza la Wafanyakazi REA liliyofanyika katika ofisi za Wakala huo Jijini Dodoma.

“Sisi pale wizarani tunasema Wizara ya Nishati ni Umeme. Tunaona mnavyofanya kazi kwa bidii. Tupo tayari kushirikiana wakati wote, ili kuhakikisha mnafikia malengo yenu vizuri,”amesema Bi. Ziana

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi Wakala wa Nishati vijijini (REA) ambaye pia ni Mkurugenzi Mkuu, Mhandisi Hassan Saidy, amesema mafanikio yaliyofikiwa na REA ni matokeo ya kufanya kazi kwa ushirikiano na bidii huku akiwataka watumishi kuendeleza umoja na kufanya kazi kwa bidii.

Akibainisha baadhi ya mafanikio yaliyofikiwa ni pamoja na ongezeko la upatikanaji na uunganishaji umeme ambapo upatikanaji wa umeme umeongezeka kutoka asilimia 69.6 mpaka 78.1 kwa maeneo ya vijijini, huku kwa nchi nzima ukiongezeka kutoka asilimia 78.4 mpaka 85.5.

Mhandisi Saidy ameongeza kuwa, kwa upande wa uungaji wa umeme umeongezeka utoka asilimia24.5 mpaka 37.1 kwa maeneo ya vijijini.

Aidha, kwa upande wa matumizi ya nishati safi ya kupikia umeongezeka kutoka asilimia 8 mpaka 23.

“Sisi tuna amini REA imechangia ongezeko la matumizi ya nishati safi ya kupikia. Matumaini ya Watanzania hasa wale wanaoishi vijijini yapo kwetu sisi Wakala wa Nishati Vijijini. Tukafanye kazi kwa bidi kuwahudumia wananchi,” amesisitiza Mhandisi Saidy.

Mwakilishi Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya Tanzania (TUGHE) Taifa, Jonas Rwegoshora amesisitiza watumishi wa REA kuwa sehemu ya mabadiliko ya mafanikio ya taasisi hiyo na kuhimiza ushirikiano wa watumishi wote kuanzia ngazi ya chini mpaka juu.






Na Said Mwishehe,Michuzi TV-Dodoma
RAIS Dk.Samia Suluhu Hassan amesema kuna mengi zaidi ambayo Serikali imejipanga kuyafanya katika kipindi cha miaka mitano ijayo huku akisisitiza ni dhima ya Serikali kuendeleza ukuaji wa Uchumi.

Hivyo amesema katika kipindi hiki Serikali itaanza utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2025 hadi 2050, ikilenga kujenga Taifa jumuishi lenye ustawi, haki na linalojitegemea.

Akizungumza Bungeni Mjini Dodoma leo Novemba 14,2025 akilihutubia Bunge la Tanzania la 13,Rais Dk.Samia amesema Dira mpya imeweka vigezo vya kuchagua sekta na maeneo ya kupewa kipaumbele yaliyobainishwa kwenye andiko la Dira yenyewe.

Amesema kati ya mikakati itakayofanyiwa kazi ni kuwekeza zaidi kwenye sekta zinazoajiri watu wengi na miongoni mwa sekta hizo ni kilimo, utalii, viwanda, ujenzi na madini.

“Malengo yetu ya kiuchumi ni kupandisha kasi ya ukuaji wa uchumi kutoka asilimia 5.6 ya sasa hadi zaidi ya asilimia 7 kuelekea mwaka 2030. Ukuaji huu utaiwezesha Serikali kuboresha huduma za kijamii na kujenga miundombinu wezeshi ya kiuchumi.

“Tutaimarisha masoko ya mitaji kwa kuhamasisha uwekezaji wa ndani, na kutumia rasilimali zetu kama madini kudhamini mikopo ya uwekezaji, badala ya kuweka mzigo mkubwa kwenye Deni la Taifa. Mwelekeo wetu ni kukua kwa pamoja kwa uchumi unaogusa maisha ya mtu mmoja mmoja na uchumi jumla.

“Mtakubaliana nami sekta binafsi ni nguzo muhimu ya ukuzaji wa uchumi, hususan Sekta Binafsi ya ndani. Tutaboresha zaidi mazingira ya biashara nchini kwa kukamilisha utekelezaji wa Mpango wa Kuboresha Mazingira ya Biashara (MKUMBI).”

Pia amesema Serikali itatekeleza mapendekezo ya Tume niliyoiunda ya Kuboresha Mifumo ya Kodi nchini ili kuwapatia wafanyabiashara wepesi katika kufanya biashara zao.

Ameongeza Serikali itaendelea kuweka nguvu zaidi kudhibiti mfumuko wa bei za bidhaa ambayo ni hatua muhimu katika kupunguza gharama za maisha kwa Wananchi.

“Pia tutaweka motisha kwa viwanda vya ndani ili viweze kuzalisha kwa gharama nafuu na kuuza kwenye soko la ndani na nje. Tutaongeza vivutio vya kikodi na visivyo vya kikodi ili kuchochea uzalishaji na kukuza ushindani wa bidhaa za ndani.

“Mbali na mikopo, tutafungua fursa mahsusi kuhamasisha vijana na wamiliki wa biashara ndogo kupata elimu ya biashara na kuweza kujisajili katika Mfumo wa Kielektroniki wa Manunuzi ya Serikali (TANSIS).”

Rais Dk.Samia amesema vile vile kupitia vyuo vyetu vya ufundi stadi VETA Serikali itaongeza programu maalum za mafunzo ya ufundi stadi na kuunganisha programu hizi na miradi ya mikakati kama reli ya kisasa (SGR), uendelezaji wa bandari, uchumi wa buluu, madini na gesi ili vijana hawa wapate uzoefu na waweze kuajirika.

Amesisitiza Serikali itaanzisha Kanda za Kuendeleza Ujuzi zitakazowawezesha vijana kupata ujuzi unaohitajika katika makampuni ya sekta binafsi, na kuangalia uwezekano wa kutoa vivutio maalum kwa makampuni yatakayotoa nafasi nyingi za ajira kwa vijana.

Aidha, wataweka mazingira ya kuhakikisha wanakuza vijana kwenye uongozi kwa kuwezesha vyuo vyetu kufanya mafunzo ya ulezi na ukuzaji wa vijana viongozi (mentorship).

“Tutataizama mikopo ya asilimia 10 ya makusanyo ya Halmashauri zetu ili kuboresha upatikanaji wa mikopo hiyo kwa walengwa. Vile vile, ni vyema walengwa wakajua kwamba Fedha hizi ni mkopo na sio msaada, ni mbegu na sio mavuno na ni mtaji na sio ruzuku, hivyo marejesho na tija yake lazima ionekane.

“Matamanio yangu ni kuona ifikapo mwaka 2030, tuwe tumetengeneza wawekezaji vijana ambao watatoa ajira kwa vijana wenzao.

Kwa kushirikiana na sekta binafsi na wadau wa maendeleo tutahamasisha ufadhili kwa biashara za wanawake…

“Ili kuwasaidia wanawake wanaofanya kazi kwenye masoko, tutaongeza na kuratibu kwa karibu Mifuko ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi ili kurasimisha biashara zao na kuwawezesha kukopesheka.”

Ameongeza Serikali itawekeza katika kuboresha miundombinu ya masoko, mifumo ya maji safi na maji taka, huduma za afya, na vituo vya matunzo ya watoto kwenye masoko.

Katika hatua nyingine, Serikali itatoa kipaumbele suala la kutenga maeneo ya biashara kwa wafanyabiashara wadogo na wa kati ili Serikali iwatambue na kuwarasimisha ili waweze kufanya kazi zao bila bughudha na wachangie kwenye Pato la Taifa.

Rais Dk.Samia amesema kwa rasilimali ambazo nchi yetu imebarikiwa na nguvu kazi kubwa tuliyonayo, anaamini tunaweza kabisa kujipanga na kufikia lengo hilo. “Kwa kufanya hivyo, ndio tutafikia lengo letu la kuzalisha ajira milioni 8.5 katika sekta mbalimbali ifikapo mwaka 2030.”

Kuhusu huduma za kijamii, amesema maendeleo makubwa yamepatikana kwenye sekta ya maji, ambapo hali ya upatikanaji wa maji ilipanda kutoka asilimia 84 hadi asilimia 91.6 mijini, na kutoka asilimia 70.1 hadi asilimia 85 vijijini.

“Tumefika pazuri kuliko pale tulipokuwa mwaka 2021. Hata hivyo, azma ya Serikali ni kufikia asilimia 100 ya upatikanaji wa maji safi, salama na uhakika. Hivyo tunakwenda kuongeza nguvu ili kuyafikia yale maeneo machache ambayo upatikanaji wa maji bado ni changamoto.

“Katika miaka 5 ijayo, tutakamilisha ujenzi wa Gridi ya Taifa ya Maji ambayo itategemea maji kutoka Ziwa Victoria, Ziwa Tanganyika na Ziwa Nyasa. Tutakamilisha miradi mikubwa ya maji inayoendelea ikiwemo miradi ya maji ya miji 28, na miradi mikubwa ya bwawa la Kiwira (itakayohudumia Mbeya).

“Bwawa la Kidunda, Bonde la Mto Rufiji (itakayohudumia Dar es Salaam, Lindi na Pwani), Same-Mwanga-Korogwe (itakayohudumia Kilimanjaro na Tanga), na upanuzi wa Capri Point (itakayohudumia Mwanza), kwa kuitaja kwa uchache.
Mkuu wa huduma za Ustawi wa Jamii jiji la Dar es Salaam, Waziri Nashiri (Katikati) akishirikiana na Mkurugenzi Mtendaji wa TAMWA, Dkt. Rose Reuben pamoja na Mwakilishi wa GIZ, Nora Loehr kukata utepe kuashiria uzinduzi wa Mradi wa "Sauti Zetu", uzinduzi huo umefanyika leo jijini Dar es Salaam leo Novemba 14, 2025.
Mkuu wa huduma za Ustawi wa Jamii jiji la Dar es Salaam, Waziri Nashiri (Katikati) akisoma kipeperushi ambacho wanawake na watoto wanatakiwa kinachotoa mwiongozo 10 ya namna ya kujilinda dhidi ya Ukatili mtandao.
Mkurugenzi Mtendaji wa TAMWA, Dkt. Rose Reuben akizungumza wakati wa uzinduzi wa Mradi wa "Sauti Zetu", uzinduzi huo umefanyika leo jijini Dar es Salaam leo Novemba 14, 2025.

Na Avila Kakingo, Michuzi Tv
CHAMA cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo la Ujerumani (GIZ) limezindua mradi uitwao “Sauti Zetu” wenye lengo la kupaza sauti za wanawake na watoto pamoja na kuelimisha jamii juu ya kupambana na ukatili wa kijinsia, hususan ule unaotokea katika majukwaa ya kidijitali. Uzinduzi huu umekuja wakati dunia ikijiandaa kuadhimisha Siku 16 za Kupinga Ukatili wa Kijinsia kuanzia Novemba 25 hadi Desemba 10.

Akizungumza katika uzinduzi huo leo Novemba 14, 2025 Mkurugenzi Mtendaji wa TAMWA, Dkt. Rose Reuben amesema kuwa ongezeko la matumizi ya mitandao ya kijamii limeambatana na changamoto kubwa za ukatili wa kidijitali unaowalenga zaidi wanawake na wasichana.

Ameeleza kuwa kundi hili bado halina uelewa wa kutosha juu ya kujilinda na kulinda taarifa zao mtandaoni, jambo linalochangia madhara ya kimwili na kisaikolojia.

"Licha ya juhudi za serikali, Umoja wa Mataifa, Umoja wa Ulaya na wadau wa maendeleo kuweka misingi ya usalama mtandaoni, bado elimu kwa jamii ni ndogo." Amesema Dkt. Rose

Pia ameeleza kuwa mifano ya vitendo vya kusambaza picha za faragha bila ridhaa, kuunda akaunti bandia, vitisho, na maudhui ya chuki kama miongoni mwa ukatili unaoongezeka nchini.

Aidha, wasichana wanaotumia majukwaa kama WhatsApp, TikTok na Snapchat wametajwa kuwa katika hatari kubwa zaidi.

Kupitia mradi huu, TAMWA imetangaza kuanza utekelezaji wa Mwongozo wa Kanuni 10 za Kujilinda na Ukatili wa Kidijitali, ambao utatumika kuongeza uelewa wa umma na kuwasaidia wanawake kujilinda dhidi ya madhila ya kimtandao. Mwongozo huo ni sehemu ya kampeni pana ya “Kupaza Sauti Ili Kupunguza Ukatili kwa Wanawake na Watoto Kupitia Vyombo vya Habari”.

Mradi wa “Sauti Zetu” unatarajiwa kutumia vyombo vya habari kama daraja muhimu kufikisha elimu kuhusu maana ya ukatili wa kijinsia, vyanzo vyake, na huduma zinazopatikana kwa waathirika.

Kupitia taarifa, vipindi, mijadala na kampeni za uelimishaji, mradi utawezesha jamii kuelewa mifumo ya kisheria, haki za waathirika na njia za kupata msaada.

Mradi unatekelezwa katika mikoa mitatu: Dar es Salaam (Kinondoni na Temeke), Dodoma (Chamwino na Bahi), na Tanga (Lushoto na Tanga Mjini).

Kwa upande wa Mwakilishi wa GIZ, Nora Loehr, akizungumza katika uzinduzi wa mradi huo amesema kuwa Mradi wa Sauti Zetu una uwezo mkubwa wa kuboresha upatikanaji wa haki kwa wanawake na watoto kupitia matumizi ya vyombo vya habari katika kutoa elimu juu ya ukatili wa kijinsia.

Amesema kuwa taarifa kupitia redio, televisheni, mitandao ya kijamii na vyombo vya habari vya jamii zinaweza kuwa mwanga muhimu kwa waathirika, hasa walioko maeneo ya vijijini ambako huduma za msaada ni adimu.

Aidha, imeelezwa kuwa kuongezeka kwa matumizi ya teknolojia kumeibua aina mpya za ukatili wa kijinsia unaofanyika mtandaoni, ikiwemo unyanyasaji wa kimtandao, usambazaji wa picha za faragha bila ridhaa, udanganyifu wa kidijitali, na matumizi ya “deepfakes”. Wanawake, wasichana, wanafunzi, waandishi wa habari na wanaharakati wameripotiwa kuwa katika hatari kubwa zaidi ya kushambuliwa kupitia majukwaa ya mtandaoni.

Hali hii imefanya elimu ya usalama wa kidijitali kuwa jambo la msingi katika mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia.

Katika jitihada za kukabiliana na changamoto hizo, TAMWA na washirika wake wamezindua kifurushi cha taarifa chenye mwongozo wa kanuni 10 za usalama mtandaoni kwa wanawake na watoto. Mwongozo huo umeandaliwa kwa lugha rahisi, ili kuwawezesha watumiaji kutambua hatari za mtandaoni, kulinda taarifa binafsi na kutumia majukwaa ya kidijitali kwa usalama zaidi.

Uzinduzi wa mradi wa Sauti Zetu umeambatana na wito wa kuimarisha mazingira salama mtandaoni na nje ya mtandao, ili kuhakikisha kuwa kila mmoja, hususan wanawake na wasichana, anaweza kusikilizwa na kupata haki.
Kwa upande wa Mkurugenzi wa WAJIKI, Janeth Mawinza amesema amesisitiza kuwa mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia yanahitaji nguvu ya pamoja, hasa katika kipindi hiki ambacho maudhui ya Siku 16 za Kupinga Ukatili wa Kijinsia yamelenga ukatili unaotokea kwenye majukwaa ya kidijitali.

Kwa ushirikiano wa wadau na nguvu ya vyombo vya habari, TAMWA inatarajia kuwa mradi huu utaongeza mwamko, kuhamasisha hatua na kuchochea jitihada za kukomesha ukatili wa kijinsia, hususan katika zama hizi za kidijitali.
Mwakilishi wa GIZ, Nora Loehr akizungumza wakati wa uzinduzi wa Mradi wa "Sauti Zetu", uzinduzi huo umefanyika leo jijini Dar es Salaam leo Novemba 14, 2025.






Picha ya pamoja.

Na Mwandishi Wetu, Morogoro.

Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) umeimarisha safu yake ya uongozi baada ya Kamishna wa Uhifadhi, Prof. Dos Santos Silayo, kuwapandisha vyeo watumishi watatu walioteuliwa kuwa Makamishna Wasaidizi, kutokana na mchango wao katika kulinda na kusimamia rasilimali za misitu nchini.

Walioinuliwa ni Mathew Ntilicha, aliyekuwa Kaimu Kamanda wa TFS Kanda ya Mashariki; Getruda Nganyagwa, aliyekuwa Kaimu Kamanda wa Kanda ya Nyanda za Juu Kusini; na Emanuel Laizer, aliyekuwa Kaimu Mkaguzi Mkuu wa Ndani. 

Watatu hao wametambuliwa kwa uadilifu, uwajibikaji na utendaji uliosaidia kupunguza vitendo vya uharibifu wa misitu katika maeneo yao.

Akizungumza kwenye hafla hiyo iliyofanyika leo Novemba 14, 2025 mjini Morogoro, Prof. Silayo aliwataka viongozi hao wapya kutekeleza majukumu yao kwa kufuata sheria, kanuni za utumishi wa umma na maadili ya taaluma, akibainisha kuwa nafasi walizopata zinahitaji uongozi thabiti na uadilifu kwa manufaa ya nchi.

“Kupandishwa cheo ni heshima, lakini pia ni wajibu mkubwa. Serikali inatarajia kuona mnatimiza majukumu yenu kwa uadilifu na uaminifu. Tunalinda rasilimali za taifa; hivyo kazi yenu ni muhimu kwa uchumi na mazingira ya nchi yetu,” alisema.

Wakati huo huo, Prof. Silayo amewataka watumishi wapya wa TFS wanaomaliza mafunzo ya awali kuwa na nidhamu, uadilifu na kuzingatia maadili ya utumishi wa umma wanapoanza utekelezaji wa majukumu yao.

Akifunga mafunzo hayo, alisema taifa linawategemea katika kulinda rasilimali za misitu na nyuki, hivyo ni muhimu wakafanya kazi kwa weledi na bila kusukumwa.

“Watumishi hawa wanakwenda moja kwa moja kazini. Ni lazima wawe na uelewa sahihi wa sheria, taratibu na maadili ya utumishi wa umma ili kutoa huduma bora kwa wananchi,” alisema Prof. Silayo.

Aliongeza kuwa TFS inaendelea kuboresha mifumo yake ili kuongeza uwazi, uwajibikaji na ubunifu katika utendaji, huku akisisitiza kuwa watumishi wapya wanapaswa kuwa mfano wa uzalendo, uaminifu na utumishi uliotukuka.

Aidha, aliwahimiza kuongeza tija kupitia maarifa waliyojifunza ili kuchochea maendeleo endelevu ya sekta ya misitu na mazingira nchini.

Hafla hizo mbili zilihudhuriwa na viongozi waandamizi wa TFS.










Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassanakiwahutubia Wabunge pamoja na viongozi mbalimbali kabla ya kufungua rasmi Bunge la 13 la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika ukumbi wa Bunge Jijini Dodoma tarehe 14 Novemba, 2025.

*Pia aelezea umuhimu wa umeme nchini katika kuleta maendeleo ya Nchi

Na Said Mwishehe,Michuzi TV-Dodoma
RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk.Samia Suluhu Hassan amesema Serikali yake eneo lingine ambalo litakaloipa uzito mkubwa ni sekta ya ujenzi na kipaumbele chao kitakuwa kukamilisha miradi mbalimbali ya ujenzi wa barabara ambazo tayari zimeanza na zinaendelea.

Amesema Serikali itaongeza kasi ya utekelezaji wa miradi ya barabara kupitia TANROADS, ili tufikie lengo letu la kuunganisha Wilaya zote na Makao Makuu ya Mikoa kwa kiwango cha lami.

Akizungumza leo Novemba 14,2025 alipokuwa akihutubua Bunge la Tanzania la 13 ambalo amelizindua rasmi Dk.Samia pamoja na kuelezea mikakati mbalimbali ya Serikali amezungumzia pia ujenzi wa miundombinu ya barabara.

Ambapo kwa Jiji la Dar es Salaam, Serikali itaboresha barabara kuu kwa kujenga barabara za juu katika makutano ya barabara katika maeneo ya Morocco, Mwenge, Magomeni na Tabata, na ujenzi wa awamu zilizobaki za miundombinu ya mabasi yaendayo haraka (BRT).

Pia wataijengea uwezo UDART ili iweze kusimamia vyema uendeshaji wa mabasi haya. Tutakamilisha pia ujenzi wa daraja muhimu, Daraja la Mto Msimbazi.

“Tutaongeza pia bajeti na uwezo wa TARURA kuboresha barabara za ndani na za vijijini ili kuhakikisha zinapitika mwaka mzima, na kuwa wakulima wanaweza kuyafikia masoko kwa urahisi.”

Kuhusu ujenzi wa makazi, amesema jitihada zao zitajielekeza kupunguza gharama za vifaa vya ujenzi ili tuwawezeshe wananchi kujenga makazi bora huku akisisitiza kuweka mkazo maalum kwenye nyumba bora na nafuu.

“Tutasimamia utekelezaji wa sera zinazolenga kuboresha hali ya makazi kwenye maeneo yenye makazi duni. Tutashirikiana na sekta binafsi ili kuongeza uwekezaji kwenye miradi ya uendelezaji miji kwa kujielekeza kwenye ujenzi wa nyumba za bei nafuu.

“Sambamba na hilo, tutaongeza kasi ya urasimishaji wa maeneo ya makazi, na kuimarisha utatuzi wa migogoro ya ardhi, kwa kupima ardhi nchi nzima kwa teknolojia ya kisasa ya satelaiti.

Wakati huo huo Dk.Samia akitoa hotuba yake Bungeni amesema pia hakuna maendeleo ya kiuchumi na kijamii bila nishati ya umeme wa uhakika na wenye nafuu.

Amefafanua katika kipindi kilichopita Serikali imeongeza kiwango cha uzalishaji wa umeme kutoka Megawati 1,600 na kufikia Megawati 4,000 na pia kufikisha miundombinu ya umeme kwenye kila kijiji.

“Tunapoelekea mwaka 2030, tumejiwekea lengo la kuongeza uzalishaji wa umeme maradufu kufikia Megawati 8,000 na tutaendelea kupanua mtandao wa umeme ili kuvifikia vitongoji vyote nchini.

“Tutaongeza uzalishaji kwa kutumia vyanzo vya nishati mbalimbali ambazo nchi yetu imebarikiwa nazo ikiwemo maji, jua, gesi, joto ardhi na upepo, na hata umeme utokanao na nguvu ya nyuklia.”

Pia amesema kupitia mpango wa Gridi Imara Serikali itakamilisha ujenzi wa miundombinu ya usafirishaji umeme na tutaongeza vituo vya kupoza umeme ili kuhakikisha shughuli za kiuchumi na makazi yanapata umeme wenye nguvu inayotakiwa.

Rais Dk.Samia amesema lengo ifikapo 2030, mikoa yote ya Tanzania iwe imeunganishwa na gridi ya Taifa ya umeme.

“Ili kuihakikishia nchi usalama wa nishati ya mafuta, tutaboresha miundombinu ya kupokea na kuhifadhi mafuta katika Bandari zetu na maeneo ya kimkakati.

“Tutasimamia utekelezaji wa Mkakati wa Nishati Safi ya Kupikia. Lengo ni kufikia asilimia 80 ya Watanzania wanaotumia Nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034, hatua itakayopunguza uharibifu wa mazingira na kulinda afya za watumiaji.

“Kwa upande wa gesi asilia, niwatoe hofu kuwa tupo kwenye hatua nzuri za majadiliano. Tuna dhamira ya dhati ni kukamilisha majadiliano hayo ya mradi huu mkubwa na wa kihistoria wa dola bilioni 42 wa uchimbaji wa gesi asilia.

“Kama tutakubaliana na wawekezaji, Mradi huo utabadilisha kabisa taswira na sura ya uchumi wetu. Katika majadiliano yetu tumechelewa kidogo kwa sababu tunahakikisha majadiliano hayo yanazingatia maslahi mapana ya nchi na kuhakikisha mradi huu utawanufaisha Watanzania moja kwa moja.

Vilevile, amesema Serikali itajielekeza pia kwenye kuongeza utafiti wa gesi asilia maeneo ya baharini na nchi kavu.


KAMPUNI inayoongoza katika michezo ya kubashiri nchini, Meridianbet Tanzania, imeendelea kudhihirisha dhamira yake ya kusaidia jamii kwa kutoa msaada wa vyakula na mahitaji muhimu kwa kituo cha MRC Rehabilitation Centre kilichopo Dar es Salaam.

Msaada huo uliojumuisha mchele, unga wa sembe, mafuta ya kupikia, sabuni za kufulia na mahitaji mengine muhimu ya nyumbani, umekabidhiwa rasmi na timu ya Meridianbet kama sehemu ya utekelezaji wa mpango wao wa Corporate Social Responsibility (CSR) wa mwezi Novemba, wenye lengo la kugusa maisha ya watu wanaokabiliana na changamoto mbalimbali za kiafya na kijamii.

Akizungumza wakati wa kukabidhi msaada huo, msemaji wa Meridianbet alisema kuwa msaada huo ni sehemu ya jitihada endelevu za Meridianbet katika kuunga mkono taasisi zinazosaidia watu wenye uhitaji maalum.

Meridianbet haikuachi nyuma, kuna michezo mbalimbali ya kasino mtandaoni pamoja na mechi za kimataifa za kubashiri zenye odds bomba zinazokuongezea nafasi ya kuongeza kipato chako kila siku. Kujiunga ni rahisi! Tembelea meridianbet.co.tz au piga *149*10#.

“Tunatambua umuhimu wa taasisi kama MRC Rehabilitation Centre katika kuwasaidia watu wanaopitia hatua za matibabu ya uraibu. Kama kampuni inayowajibika kijamii, tumeona ni vyema kushiriki katika kuhakikisha wanaoishi kwenye kituo hiki wanapata mahitaji ya msingi kama chakula na usafi,” alisema.

Kwa upande wao, viongozi wa MRC Rehabilitation Centre waliishukuru Meridianbet kwa moyo wa upendo na kujitoa kusaidia jamii, wakieleza kuwa msaada huo umefika kwa wakati ambapo kituo kinahitaji sana rasilimali za kusaidia wahusika wanaopatiwa huduma za ukarabati.

“Tunashukuru sana Meridianbet kwa msaada huu. Umekuja wakati sahihi na utasaidia sana kuhakikisha wale tunaowahudumia wanapata mahitaji ya msingi. Tunathamini sana ushirikiano huu na tunatarajia kuendelea nao,” alisema mmoja wa viongozi wa kituo hicho.


Meridianbet imekuwa mstari wa mbele katika kusaidia jamii kupitia miradi mbalimbali ya kijamii, ikiwemo kusaidia vituo vya watoto yatima, hospitali, shule, na vikundi vya jamii vinavyolenga ustawi wa wananchi.
*Asema wengi walifuata mkumbo Oktoba 29,atoa maelekezo kuangaliwa viwango vya makosa

*Asisitiza kama Taifa linaendelea kujifunza na kujirekebisha,aizungumzia demokrasia 

Na Said Mwishehe,Michuzi TV-Dodoma

RAIS Dk.Samia Suluhu Hassan amesema katika vurugu zilizotokea Oktoba 29 mwaka huu wapo vijana wengi ambao wamekamatwa na kushtakiwa kwa makosa ya uhaini kwatojua wanachokifanya hivyo ametangaza msamaha kulingana na kiwango cha makosa yaliyofanywa ba vijana hao.

Amefafanua kuna wakati vijana hufuata mkumbo wa uhalifu kwa ushabiki, hivyo anatambua kwamba vijana wengi waliokamatwa na kushtakiwa kwa makosa ya uhaini hawakujua wanachokifanya. 

Akizungumza leo Novemba 14,2025 Bungeni Mjini Dodoma alipokuwa akilihutubia Bunge la Tanzania la 15 Kama ishara ya kulizindua rasmi Rais Dk.Samia amesema akiwa Mama na Mlezi wa Taifa hili, anavielekeza  vyombo vya sheria na hasa Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka kuangalia kiwango cha makosa yaliyofanywa na vijana hao.

“Kwa wale ambao wanaonekana walifuata mkumbo na hawakudhamiria kufanya uhalifu wawafutie makosa yao. Ninatoa msamaha huo kwa sababu, hata maneno ya Mungu katika Kitabu cha LUKA sura ya 23 Mstari wa 34 yanasema, na hapa nanukuu: “Yesu akasema, Baba uwasamehe kwa kuwa hawajui watendalo.”

“Ndugu zangu Watanzania, tujifunze kutokana na mapito yetu, hapana shaka kwamba Tanzania ni nchi inayofuata misingi ya kidemokrasia, ila, demokrasia kamili inaweza kutafsiriwa kwenye mitazamo tofauti (haina formula moja). 

“Kama Taifa tunaendelea kujifunza na kujirekebisha. Hivyo basi, sote kwa umoja wetu tunapaswa tuitumie fursa hii tuendelee kujifunza, tujirekebishe na tukubaliane jinsi ya kuiendesha nchi yetu kidemokrasia kwa kuzingatia tamaduni, mila na desturi zetu na sio za kuletewa.”

Akieleza zaidi Rais Dk.Samia amesema kama walivyoagizwa na Ilani ya CCM ya mwaka 2025 hadi 2030, moja ya hatua itakayotufikisha kwenye maelewano hayo ni marekebisho ya Katiba yetu. 

Ameongeza kwamba Serikali imeahidi kuanza kulifanyia kazi suala la mabadiliko ya Katiba ndani ya siku mia za muhula wa pili wa Awamu ya Sita kwa kuanza na Tume ya Usuluhishi na Maelewano.

“Tunapozungumzia umoja wa Kitaifa tunaongozwa na uwepo wa Tunu ya Muungano wetu. Hivyo basi, kuudumisha kuimarisha na kuuenzi Muungano wetu kutaendelea kuwa kipaumbele cha Serikali tunayoiunda. 

“Tutaendelea kuchukua hatua madhubuti kuhakikisha tunatatua changamoto za Muungano kila zinapojitokeza.

Kuhusu Serikali ya Awamu ya sita ameliambia Bunge kwamba iliendeleza waliyoyaanza  katika awamu wa tano, na hivyo kaulimbiu yake ilikuwa 'Kazi Iendelee'. 

“Ninyi ni mashahidi kuwa kazi iliendelezwa na mengi yalikamilishwa, kama nilivyoeleza katika hotuba ya kufunga Bunge la 12 la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tarehe 27 Juni mwaka huu 2025. Niwahakikishie katika miaka mitano ijayo tutalinda na kuendeleza mafanikio haya pamoja na kuleta mafanikio mengine na makubwa zaidi.”
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassanakiwahutubia Wabunge pamoja na viongozi mbalimbali kabla ya kufungua rasmi Bunge la 13 la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika ukumbi wa Bunge Jijini Dodoma tarehe 14 Novemba, 2025.




Na Said Mwishehe,Michuzi TV-Dodoma

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk.Samia Suluhu Hassan ametoa rai kwa vijana wa Taifa hili wasikubali hata siku moja kushawishiwa kuichoma nchi yao wenyewe na kusisitiza wasikubali kukata tawi la mti ambao wameukalia.

Akizungumza leo Bungeni Mjini Dodoma alipokuwa akizindua Bunge la Tanzania la 13,Rais Dk.Samia ambaye ametoa muelekeo wa masuala mbalimbali yatakayotekelezwa na Serikali ya Sita ametumia nafasi hiyo kuelezea uvunjifu wa amani uliotokea Oktoba 29 mwaka huu.

“Pamoja na kuwa uchaguzi umefanyika kumewepo na uvunjifu wa amani ambao umesababisha uharibifu wa mali na upotevu wa maisha na kuharisha usalama wa nchi.

“Tunapoenda mbele niwasihi sana watanzania tuongozwe na dhamira ya maelewano ,ushirikishwaji ,kujirekebisha na umoja.

“Kwa wanangu vijana wa Taifa hili la Tanzania nchi hii imejengwa kwenye misingi ya amani na utulivu wa kisiasa.Sisi wazazi wenu tungeshawishika kufanya mliyofanya wakati huu nchi hii isingekuwa na neema na maendeleo mnayoyaona leo.

“Nataka kurudia hilo kwa wanangu vijana wa Taifa la Tanzania sisi wazazi wenu kama tungefanya mliyoyafanya ninyi nchi hii isingekuwa na neema na maendeleo mnayoyaona .

“Hivyo niwasihi sana wanangu vijana wa Tanzania .Nchi hii ni yenu ,shida zozote zinazowakabili msikubali hata siku moja kushawishiwa kuic
homa nchi yenu wenyewe .Msikubali kukata tawi la mti ambao umekalia.”
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassanakiwahutubia Wabunge pamoja na viongozi mbalimbali kabla ya kufungua rasmi Bunge la 13 la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika ukumbi wa Bunge Jijini Dodoma tarehe 14 Novemba, 2025.





Top News