Katika juhudi za kuhakikisha Tanzania inafikia azma ya kuwa nchi ya kijani ifikapo mwaka 2050, Shirika la INADES-Formation Tanzania kwa kushirikiana na Ofisi ya Makamu wa Rais – Idara ya Mazingira limeandaa kikao kazi cha kuandaa Mpango wa Usimamizi wa Mazingira wa Wilaya ya Bahi, kwa kushirikisha wataalamu kutoka Wilaya za Chemba na Kondoa.

‎Akifungua kikao hicho Leo katika ofisi ya Makamu wa Rais, Mtumba mjini Dodoma, Kaimu Mkurugenzi wa Mazingira kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais – Idara ya Mazingira, Dk. Paul Deogratius, alisema ushiriki wa Wilaya za Chemba na Kondoa utasaidia kubadilishana uzoefu katika mchakato wa kuandaa mpango huo kwa Wilaya ya Bahi.

‎‎Alieleza kuwa mipango ya usimamizi wa mazingira katika ngazi ya wilaya ni takwa la kisheria na ni nyenzo muhimu katika kukabiliana na changamoto mbalimbali za mazingira zinazozikabili halmashauri nchini.

‎"Kitaifa, zimetambuliwa zaidi ya changamoto 13 za mazingira, huku kila wilaya ikiwa na changamoto zake kulingana na mazingira na shughuli za kiuchumi zinazofanyika katika eneo husika. Hivyo, uwepo wa mpango wa usimamizi wa mazingira ni muhimu katika kutoa mwongozo wa namna ya kuzikabili changamoto hizo," alisema Dk. Deogratius.

‎‎Aliongeza kuwa maandalizi ya mpango huo yataisaidia Tanzania kutekeleza mikakati ya kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi na kufikia lengo la kuwa nchi ya kijani ifikapo mwaka 2050.

‎‎Kwa upande wake, Mkurugenzi wa INADES-Formation Tanzania, Bi. Jacqueline Nicodemus, alisema ushirikiano na Ofisi ya Makamu wa Rais – Idara ya Mazingira ni muhimu ili kuhakikisha mipango hiyo inaandaliwa kwa kuzingatia miongozo, sera na mikakati ya kitaifa ya usimamizi na uhifadhi wa mazingira.

‎Aidha, aliomba Ofisi hiyo kushiriki katika uzinduzi wa mipango ya usimamizi wa mazingira ya Wilaya za Chemba na Kondoa, akisema ushiriki huo utatoa msukumo na kuhamasisha wadau mbalimbali kutambua umuhimu wa kuhifadhi mazingira kwa maendeleo endelevu ya nchi.

‎‎Nao washiriki wa kikao hicho walisisitiza kuwa mipango ya usimamizi wa mazingira katika wilaya hizo inapaswa kuendana na vipaumbele vya kitaifa, ikiwemo Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, mipango kabambe ya maendeleo, Sera ya Taifa ya Mazingira pamoja na miongozo mingine ya uhifadhi wa mazingira.

‎‎Vilevile, walieleza umuhimu wa kupata mwongozo wa kitaalamu kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais – Idara ya Mazingira katika hatua za kuandaa na kupitia rasimu ya Mpango wa Usimamizi wa Mazingira wa Wilaya ya Bahi, ili kuhakikisha unakidhi viwango na matakwa ya kitaifa.








Na Mwandishi wetu, Dar es Salaam

Mwenyekiti wa Bodi ya Ofisi ya Hakimiliki Tanzania (COSOTA), Victor Tesha, amewataka wanakwaya wa Flying Family Choir (FFC) kuanzisha miradi ya maendeleo itakayokuwa chanzo cha kuongeza kipato na kuwasaidia kujikomboa kutoka katika umaskini.

Tesha amesema hayo jana, Jumapili, katika tamasha la kwaya hiyo lijulikanalo FFC Corporate Encore 2026, lililofanyika katika Ukumbi wa Cardinal Rugambwa, Oysterbay, jijini Dar es Salaam, na kuhudhuriwa na watu mbalimbali, akiwemo Askofu wa Jimbo Katoliki la Morogoro, Lazarus Msimbe.

FFC Kwaya inaundwa na wanakwaya kutoka madhehebu matatu ya Kikristo ambayo ni Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Kanisa la Anglikana na Kanisa Katoliki, wakishirikiana kupitia huduma ya uimbaji wa injili.

Akizungumza katika tamasha hilo, Tesha ambaye pia ni Makamu wa Rais wa Shirikisho la Vyama vya Wachimbaji Wadogo wa Madini Tanzania (FEMATA), amesema wanakwaya wengi bado wanakabiliwa na changamoto za kiuchumi na hali zao za maisha si za kuridhisha, hivyo kuna umuhimu wa kuwa na mradi endelevu utakaoweza kuwanufaisha hata katika kipindi cha miaka 10 ijayo.

Amesema uwepo wa mradi mkubwa wa kwaya utasaidia kujenga ustawi wa wanakwaya na kuhakikisha huduma ya uinjilishaji inaendelea sambamba na kuimarika kwa maisha yao ya kiuchumi.

"Ningependa kuona wanakwaya wakifikiria zaidi kuhusu uwekezaji na miradi itakayowasaidia kujikomboa kiuchumi. Wengi bado hali zao si nzuri, hivyo tunahitaji kuwa na mradi ambao hata baada ya miaka 10 utakuwa umebadilisha maisha ya wanakwaya," amesema Tesha.

Aidha, ameahidi kukaa pamoja na bodi ya kwaya hiyo ili kujadili namna bora ya kupata mradi mkubwa na wenye tija ambao utalenga kuinua vipato vya wanakwaya na kuimarisha ustawi wao wa kiuchumi.

Kwa upande wake, Katibu wa kwaya hiyo, Brigita James amesema pamoja na kwaya hiyo kumiliki vifaa vyake vya muziki, bado inahitaji kuwa na chombo chake cha usafiri kitakachorahisisha shughuli za uinjilishaji na usafiri wa wanakwaya wanapopata mialiko ya kuhudumu katika maeneo mbalimbali.

Amesema upatikanaji wa chombo hicho utapunguza gharama za usafiri na kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa shughuli za kwaya, hususan katika huduma za uinjilishaji zinazofanyika ndani na nje ya Dar es Salaam.

Naye Mwenyekiti wa kwaya hiyo, Innocent Fundisha amesema kwaya hiyo imefanikiwa kufanya matamasha 10 tangu kuanzishwa kwake, jambo linalowapa fahari kutokana na kuendelea kudumu katika upendo, amani na mshikamano miongoni mwa wanakwaya wake.

Fundisha amesema wanakwaya wa FFC wanatoka katika madhehebu matatu ya Kikristo ambayo ni KKKT, Anglikana na Kanisa Katoliki, lakini tofauti zao za kimadhehebu hazijawahi kuwa kikwazo katika huduma yao ya uimbaji.

Amesema umoja, upendo na mshikamano walioujenga ni ishara kuwa licha ya kutofautiana madhehebu, wote wanamuabudu Mungu mmoja katika roho na kweli, huku wakitumia muziki wa injili kuhubiri amani na kuimarisha ushirikiano miongoni mwa waumini.









Jeshi la Polisi Tanzania lingependa kujulisha kuwa, Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, IGP Camillus Wambura, amemhamisha Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Twaha Juma Lulengelule ambaye alikuwa Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (RCO) Mkoa wa Tabora kuwa Kamanda wa Polisi (RPC) Mkoa wa Tabora.


Uhamisho huo umefanyika ili kujaza nafasi iliyokuwa wazi baada ya aliyekuwa Kamanda wa Polisi Mkoa huo, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Richard George Abwao, kufariki dunia Juni 20, 2026.


Imetolewa na;

Msemaji wa Jeshi la Polisi

Makao Makuu ya Polisi

Dodoma,Tanzania

Na Mwandishi Wetu
NDOTO za vijana wa Tanzania wanaotarajia kujiunga na vyuo vikuu mbalimbali nje ya nchi kwa mwaka wa masomo 2026/2027 zimeingia hatua muhimu baada ya Global Education Link kuwakutanisha wanafunzi hao pamoja na wazazi na walezi wao kwa ajili ya kuhakiki nyaraka na kukamilisha maandalizi ya safari.
Kikao hicho kilichofanyika katika Makao Makuu ya Global Education Link, Dar es Salaam, kililenga kuhakikisha kila mwanafunzi anakuwa na nyaraka sahihi, taarifa za kutosha na maandalizi muhimu kabla ya kuondoka nchini kwenda kuanza masomo.

Akizungumza katika mkutano huo, Mkurugenzi Mtendaji wa Global Education Link, Abdulmalik Mollel, alisema lengo kuu la kikao hicho ni kuhakiki na kukamilisha nyaraka muhimu za wanafunzi, kujibu maswali ya wazazi na kuhakikisha changamoto zinazoweza kuchelewesha safari zinapatiwa ufumbuzi mapema.

Mollel alisema wazazi na walezi wanapaswa kujiridhisha kuhusu utambuzi wa kisheria wa chuo kilichochaguliwa kwa kupata uthibitisho rasmi kutoka Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania, ili kuhakikisha sifa zitakazopatikana baada ya kuhitimu zinatambuliwa na mamlaka husika nchini.

Kwa mujibu wa Mollel, safari ya masomo nje ya nchi haiishii katika kupata nafasi ya kujiunga na chuo pekee, bali inahitaji maandalizi kuhusu visa, malazi, usafiri, usalama, sheria, utamaduni wa nchi husika na uwezo wa mwanafunzi kuishi kwa nidhamu na uwajibikaji.

Kwa upande wao, wazazi na walezi walioshiriki kikao hicho walisema wameridhishwa na namna Global Education Link ilivyowahudumia na kuwapatia majibu kuhusu hatua mbalimbali za udahili na maandalizi ya safari.
Mmoja wa walezi hao, Asuba Omary kutoka Zanzibar, alisema kikao hicho kimemsaidia kufahamu mambo ya kuzingatia kabla ya mzazi kuamua kumsomesha mtoto katika chuo kikuu cha nje ya Tanzania.






Mkuu wa Kitengo cha Biashara wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Victor Nchimbi akizungumza na baadhi ya wajasiriamali kuhusu huduma zinazotolewa na benki hiyo hususani zinazowalenga wafanyabiashara wadogo na wa kati, katika hafla ya Maadhimisho ya Siku ya Wajasiriamali Duniani ambayo Absa ilikuwa moja ya taasisi zilizojitokeza kudhamini tukio hilo, jijini Dar es Salaam hivi karibuni. Tukio hili liliwakutanisha zaidi ya wajasiriamali 350, viongozi wa sekta, na watunga sera chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara ili kushirikiana katika kuendeleza ukuaji wa biashara zinazochochea injini ya uchumi wa taifa.

Meneja Bidhaa wa Kitengo cha Biashara wa Benki ya Absa Tanzania, Bi. Devroda Kagusa (kulia) akizungumza kuhusu huduma zizotolewa na benki hiyo hususani zinazowalenga wafanyabiashara wadogo na wa kati, kwa baadhi ya wahudhuriaji waliofika katika banda lao, katika Maadhimisho ya Siku ya Wajasiriamali Duniani ambayo Absa ilikuwa moja ya taasisi zilizojitokeza kudhamini, jijini Dar es Salaam hivi karibuni. Tukio hili liliwakutanisha zaidi ya wajasiriamali 350, viongozi wa sekta, na watunga sera chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara ili kushirikiana katika kuendeleza ukuaji wa biashara zinazochochea injini ya uchumi wa taifa.





Ofisa Huduma kwa Wateja wa Benki ya Absa, Bi. Mboni Sabura (katikati) akizungumza na baadhi ya wajasiriamali kuhusu huduma zinazotolewa na benki hiyo hususani akaunti maalumu ya wanawake ya She, katika hafla ya Maadhimisho ya Siku ya Wajasiriamali Duniani ambayo Absa ilikuwa moja ya taasisi zilizojitokeza kudhamini, jijini Dar es Salaam hivi karibuni.Kulia ni Meneja Bidhaa Kitengo cha Biashara wa Benki ya Absa Tanzania, Bi. Devroda Kagusa. Tukio hili liliwakutanisha zaidi ya wajasiriamali 350, viongozi wa sekta, na watunga sera chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara ili kushirikiana katika kuendeleza ukuaji wa biashara zinazochochea injini ya uchumi wa taifa.






Meneja Bidhaa wa Kitengo cha Biashara wa Benki ya Absa Tanzania, Bi. Devroda Kagusa (kulia) akizungumza kuhusu huduma zizotolewa na benki hiyo hususani zinazowalenga wafanyabiashara wadogo na wa kati, kwa baadhi ya wajasiriamali waliofika katika Maadhimisho ya Siku ya Wajasiriamali Duniani, ambayo Absa ilikuwa moja ya taasisi zilizojitokeza kuwezesha tukio hilo, jijini Dar es Salaam hivi karibuni. Tukio hili liliwakutanisha zaidi ya wajasiriamali 350, viongozi wa sekta, na watunga sera chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara ili kushirikiana katika kuendeleza ukuaji wa biashara zinazochochea injini ya uchumi wa taifa.


Baadhi ya wawezeshaji na wajasiriamali waliojitoleza kushiriki Maadhimisho ya Siku ya Wajasiriamali Duniani wakipiga picha ya pamoja mara baada ya kukamilika kwa tukio hilo, jijini Dar es Salaam hivi karibuni. Benki ya Absa ilikuwa moja ya taasisi zilizojitokeza kudhamini hafla hiyo. Tukio hili liliwakutanisha zaidi ya wajasiriamali 350, viongozi wa sekta, na watunga sera chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara ili kushirikiana katika kuendeleza ukuaji wa biashara zinazochochea injini ya uchumi wa taifa.








Na Farida Mangube, Morogoro
Wataalamu wa saikolojia nchini wameeleza kuwa ukosefu wa tafiti zinazoakisi uhalisia wa jamii za Kitanzania, pamoja na kuendelea kutegemea nadharia za Magharibi, bado ni kikwazo kikubwa katika juhudi za kukabiliana na changamoto za afya ya akili zinazoongezeka nchini.

Kauli hiyo imetolewa katika Kongamano la Tatu la Kisayansi na Mkutano Mkuu wa 10 wa Chama cha Wanasaikolojia Tanzania (TAPA) unaoendelea mkoani Morogoro, ambapo washiriki wamesisitiza umuhimu wa kuwekeza katika tafiti zinazozingatia mazingira, tamaduni na mahitaji halisi ya jamii za Kitanzania ili kuboresha elimu ya saikolojia na huduma za afya ya akili.

Akizungumza nje ya mkutano huo uliuokwenda sambamba na uchaguzi Rais mpya wa TAPA Barnabas Nkinga amesema chama kitaendelea kuhamasisha tafiti za kisayansi zinazolenga mazingira ya Tanzania, kuimarisha ushirikiano kati ya wataalamu na taasisi mbalimbali, pamoja na kuhakikisha maazimio ya kongamano hilo yanatekelezwa kwa vitendo.

Amesema tafiiti zitasaidia kuifanya taaluma ya saikolojia kutoa suluhisho yanayokidhi changamoto zinazowakabili wananchi na kuchangia katika kuboresha huduma za afya ya akili nchini.

Baadhi ya washiriki wa kongamano hilo akiwemo Charles Deogratius wameitaka Serikali na wadau wa sekta ya afya kuongeza uwekezaji katika tafiti za ndani, wakisema utegemezi wa nadharia za Magharibi pekee umekuwa ukikwamisha upatikanaji wa mbinu zinazolingana na mazingira ya Kitanzania.

Pia wameutaka uongozi mpya wa TAPA kusimamia kwa karibu utekelezaji wa maazimio yatakayopitishwa ili taaluma ya saikolojia iweze kutoa mchango mkubwa zaidi katika kukabiliana na changamoto za afya ya akili nchini.

Kongamano la Tatu la Kisayansi pamoja na Mkutano Mkuu wa 10 wa Chama cha Wanasaikolojia Tanzania limehitimishwa kwa kupitisha maazimio yatakayokuwa mwongozo wa kuimarisha tafiti, elimu ya saikolojia na huduma za afya ya akili nchini. Uongozi mpya wa chama unatarajiwa kuanza rasmi kuyasimamia na kuyatekeleza maazimio hayo.







Na Mwandishi Wetu
UJUMBE wa walimu na viongozi wa elimu kutoka Mkoa wa Dodoma wapatao 40 umeondoka kwenda Korea Kusini kujifunza mbinu za kisasa za ufundishaji, usimamizi wa shule na matumizi ya teknolojia katika elimu.

Walimu hao wanatarajiwa kushiriki mafunzo na ziara ya kielimu ya siku nne ikiwa ni sehemu ya kutambua mchango wao katika kuongeza ufaulu wa wanafunzi mkoani humo.

Mratibu wa safari hiyo na Mkurugenzi Mtendaji wa Global Education Link, Abdulmalik Mollel, amesema walimu hao waliondoka kupitia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere kuelekea Seoul, Korea Kusini, kupitia Doha, Qatar.

Amesema katika ziara hiyo washiriki watajifunza namna Korea Kusini inavyotumia teknolojia, ubunifu, nidhamu na usimamizi bora katika kuimarisha ufundishaji na ujifunzaji. Pia watapata uzoefu kuhusu matumizi ya mifumo ya kidijitali darasani, maandalizi ya masomo na ufuatiliaji wa maendeleo ya wanafunzi.

Amesema kabla ya kuondoka walipatiwa mafunzo ya maandalizi kuhusu utamaduni wa Korea Kusini, utunzaji wa muda na wajibu wao kama wawakilishi wa Mkoa wa Dodoma na Tanzania.

Amesema lengo la safari hiyo si kutembelea Korea Kusini pekee, bali kujifunza uzoefu wa kimataifa utakaosaidia kuboresha ufundishaji, usimamizi wa shule na kuongeza ufaulu wa wanafunzi watakaporejea nchini.

Amesema mpango huo umetokana na jitihada za Mkoa wa Dodoma za kutambua na kuwapa motisha walimu walioonesha utendaji bora, baada ya Mkutano wa Wadau wa Elimu uliowakutanisha viongozi wa Serikali, walimu, maofisa elimu, sekta binafsi na wadau wengine wa maendeleo ya elimu.

Amesema safari hiyo imefanikishwa kupitia ushirikiano wa Serikali ya Mkoa wa Dodoma na wadau mbalimbali, wakiwemo Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF), Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), Benki ya NMB na Global Education Link, ikiwa ni sehemu ya kuendeleza maendeleo ya kitaaluma kwa walimu na kuboresha sekta ya elimu.





Serikali imeonya taasisi za umma zinazofanya vibaya kujitathmini na kuchukua hatua za haraka za kuboresha utendaji wao, ikisisitiza kuwa haitavumilia taasisi zitakazoendelea kuonesha utendaji duni kwa muda mrefu.

Onyo hilo lilitolewa na Msajili wa Hazina, Bw. Nehemiah Mchechu, jijini Dar es Salaam Ijumaa, Juni 26, 2026, wakati wa mahojiano maalumu kuelekea Siku ya Gawio itakayofanyika Jumanne, Juni 30, 2026, katika Ikulu ya Dar es Salaam.

Bw. Mchechu alisema taasisi zote zinazostahili kuwasilisha gawio na michango mingine Serikalini zinapaswa kutekeleza wajibu huo kwa wakati, akisisitiza kuwa kushindwa kufanya hivyo ni kuinyima Serikali na wananchi mapato stahiki.

“Mashirika si mali ya bodi za wakurugenzi wala menejimenti; ni mali ya umma zinazosimamiwa na Serikali. Kwa muktadha huo, kurejesha kilicho haki ya wananchi si fadhila, bali ni wajibu,” alionya.

Alisisitiza kuwa viongozi wa taasisi za umma wanapaswa kuhakikisha malengo ya faida wanayopewa yanafikiwa ili kuongeza mchango wa taasisi hizo kwa uchumi wa taifa.

“Lazima taasisi zetu ziyaishi malengo ya faida ambayo huwa tunazipa. Mtu (kiongozi wa taasisi) ambaye ataendelea kushindwa kuleta gawio kwa kipindi kirefu, huyo hatufai,” alionya Bw. Mchechu.

Aidha, alisema gawio na michango mingine inapaswa kutokana na faida au ziada halisi ya taasisi, badala ya kukopa fedha, akisisitiza kuwa kufanya hivyo kunatoa taswira isiyo sahihi kuhusu utendaji wa taasisi.

“Ukikopa ili utoe gawio au mchango mwingine kwa Serikali, unakuwa unamdanganya Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, na hata nafsi yako mwenyewe,” alisema.

Alipoulizwa iwapo taasisi zitakazoshindwa kufanya vizuri katika utoaji wa gawio mwaka huu zinaweza kufutwa, Bw. Mchechu alisema kufutwa au kuunganishwa kwa taasisi za umma ni mchakato endelevu unaofuata taratibu zilizowekwa, na si uamuzi unaotokana na matokeo ya Siku ya Gawio pekee.

“Hatufuti taasisi kwa sababu ya matokeo ya siku ya gawio. Tunazipa kwanza muda wa kufanya maboresho, na zisipoonyesha mabadiliko ndipo tunachukua hatua stahiki,” alifafanua Bw. Mchechu.

Katika mwaka wa fedha 2024/25, Ofisi ya Msajili wa Hazina (OTR) ilikusanya Sh1.028 trilioni kama gawio na michango mingine kutoka kwa taasisi za umma pamoja na kampuni ambazo Serikali ina umiliki wa hisa chache, kiwango kilichoweka rekodi mpya tangu kuanzishwa kwa ofisi hiyo mwaka 1959.

Pamoja na mafanikio hayo, Bw. Mchechu alisema Serikali inaamini bado kuna fursa kubwa ya kuongeza makusanyo kwa kuimarisha utendaji wa taasisi za umma na usimamizi wa uwekezaji wa Serikali.

Akizungumzia matarajio ya siku zijazo, alisema OTR inaamini kuwa maboresho yanayoendelea katika ufanisi wa kiutendaji na kifedha wa taasisi za umma yataonekana katika matokeo ya mwaka huu wa fedha, huku mafanikio zaidi yakitarajiwa katika miaka ijayo.

“Tunategemea tutaanza na nguvu mpya, mwaka huu tutavunja rekodi ya mwaka jana na mwakani tutavunja rekodi ya mwaka huu,” alisema Bw. Mchechu.

Kauli za Bw. Mchechu zinaendana na msimamo wa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, Mhe. Prof. Kitila Mkumbo, ambaye hivi karibuni alionya taasisi na mashirika ya umma yanayoendelea kuonesha utendaji usioridhisha kuwa yako hatarini kufutwa au kuunganishwa endapo hayataboresha utendaji wake.

Prof. Mkumbo alisema haiingii akilini kuona baadhi ya mashirika ya umma yakishindwa kutoa gawio stahiki licha ya uwekezaji mkubwa uliofanywa na Serikali.

Alisema Serikali itazipa taasisi husika muda wa kujirekebisha kabla ya kuchukua maamuzi ya kuziunganisha au kuzifuta pale itakapobidi.

“Ni afadhali kuwa na mashirika machache ya biashara, lakini yanayotoa gawio stahiki kwa Serikali,” alisisitiza Prof. Mkumbo.

Kwa mujibu wa OTR, Serikali inamiliki hisa katika taasisi na kampuni 308, ambapo 91 zinafanya shughuli za kibiashara huku 217 zikitoa huduma za umma.

Prof. Mkumbo alisema Serikali inataka kuona wananchi wakinufaika zaidi na uwekezaji wa Sh92.3 trilioni uliofanywa katika mashirika na taasisi za umma.

Ili kufanikisha azma hiyo, OTR imesema inaendelea kuimarisha usimamizi wa utendaji wa taasisi za umma ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma na usimamizi wa uwekezaji.

Bi. Lightness Mauki, Mkurugenzi wa Usimamizi wa Utendaji, Ufuatiliaji na Tathmini ya Mashirika ya Kibiashara wa OTR, alisema ofisi hiyo imejipanga kuendelea kuimarisha utendaji wa taasisi za umma kwa lengo la kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma na usimamizi wa uwekezaji.

“Ni imani yetu kuwa usimamizi bora wa utendaji wa taasisi za umma ni msingi wa kuleta mageuzi endelevu katika uendeshaji wa taasisi na mashirika ya umma,” alisema Bi. Mauki.

Alisema usimamizi huo unatarajiwa kuchochea uzalishaji, kukuza uchumi na kuongeza mapato ya kodi na yasiyo ya kodi, hatua itakayoimarisha uwezo wa serikali kutekeleza majukumu yake ya maendeleo na kutoa huduma bora kwa wananchi.

Kwa upande wake, Bw. David Shambwe, Mkurugenzi wa Usimamizi wa Mashirika Yasiyo ya Kibiashara wa OTR, alisema pamoja na mashirika hayo kutokuwa na lengo la kuzalisha faida, yanapaswa kuonyesha ufanisi katika utoaji wa huduma na matumizi ya rasilimali za umma.

Alisema OTR inaendelea kuimarisha mifumo ya ufuatiliaji na tathmini ya utendaji ili kuhakikisha mashirika hayo yanatekeleza majukumu yake kwa ufanisi, uwajibikaji na kwa kuzingatia thamani ya fedha katika matumizi ya rasilimali za Serikali.

“Lengo letu ni kuona mashirika yasiyo ya kibiashara yanatoa huduma bora, zenye tija na zinazokidhi matarajio ya wananchi. Ufanisi wa taasisi hizi ni sehemu muhimu ya kuhakikisha uwekezaji wa Serikali unaleta matokeo chanya kwa maendeleo ya taifa,” alisema Bw. Shambwe.

Msajili wa Hazina, Bw. Nehemiah Mchechu, akizungumza na Mwandishi wa Habari wa Azam TV, Kissa Daniel, wakati wa mahojiano maalum yaliyofanyika Ijumaa iliyopita katika makao makuu ya Ofisi ya Msajili wa Hazina, jijini Dar es Salaam."

NA MWANDISHI WETU


VETERANI wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM), wamesema wataendelea kuenzi mchango mkubwa wa aliyekuwa Mwenyekiti wa Baraza la Wazee wa CCM, Mkoa wa Dar es Salaam, marehemu Mohammed Mtulia.

Ahadi hiyo ilitolewa na Veterani Sadick Chamumi, kwa niaba ya Katibu wa Maveterani hao, Mkoa wa Dar es Salaam, walipofika nyumbani kwa marehemu Mzee Mtulia, Mtaa wa Muheza, wilayani Temeke, kuwasilisha rambirambi zao.

"Mzee Mtulia ameacha wasifu mkubwa, hivyo inabidi tujifunze kutoka kwake. Kwa niaba ya Mavetarani wa UVCCM, tunaipa pole familia na tutaendelea kushirikiana nayo,”almesema Chamumi.

Mzee Mtulia alifariki dunia Mei 5, mwaka huu, nyumbani kwake Mtaa wa Mkuranga B, wilayani Temeke.

Naye, Katibu Msaidizi wa Veterani wa UVCCM, Mkoa wa Dar es Salaam, Justy Mboke, ameeleza Mzee Mtulia enzi za uhai wake alifanya mambo makubwa, hususan kuimarisha mabaraza ya wazee kuanzia ngazi za tawi, kata, wilaya hadi mkoa.

“Mabaraza hayo mpaka hivi sasa yanafanya kazi. Sifa hiyo tutaiheshimu na kuienzi sisi veterani,” amesema.

Kwa upande wake, Katibu wa Baraza la Wazee wa CCM, Mkoa wa Dar es Salaam, Mzee Mohammed Mbonde, amewashukuru veterani kwa kuwasilisha rambirambi.

“Mzee Mtulia alifundisha upendo, uelewano, kuheshimiana, kuthaminiana na kuvumiliana. Haya ndiyo yalikuwa malezi yake kwetu,” amesema na kuongeza kuwa tukio hilo ni la udugu zaidi na upendo.

Amewaomba wazee hao kuendelea kushirikiana na kushikamana kwa kuwa uzee ni udugu, busara na hekima.

Msemaji wa familia ya marehemu Mtulia,ambaye ni mtoto wa marehemu, Athuman Mtulia, alishukuru veterani kwa kumuenzi Mzee Mtulia, kwa kuwa kitendo hicho kimeleta faraja katika familia.

Veterani ni watu wote ambao wakuliwa TANU Youth Legue na Afro Shiraz Party Legue, waliotikia wito wa Baba wa Taifa hayati Mwalimu Julius Nyerere kutaka vijana wajiunge na Jeshi jipya la Tanganyika mwaka 1964 na waliotembea kwa miguu kuunga mkono Azimio la Arusha.

Pia wale wote walioshiriki vita ya Kagera dhidi ya Fashti Nduli Amin na ambao walikuwa vijana wa CCM waliovuka umri kwa mujibu wa kanuni toleo la Mwaka 1978 ukomo wa kuwa kijana wa miaka 35 ni veterani wa Chama.

Dhumuni ni kutayarisha veterani vijana wa kuwa watetezi na walinzi wa CCM na serikali yake kwa vitendo ambapo kariri ya vetenari hao ni Ujamaa na Kujitegemea.





Na. Saidina Msangi na Asia Singano, WF – Dar Es Salaam

Wizara ya Fedha imetoa wito kwa wananchi, wafanyabiashara, na wadau mbalimbali wa uchumi kutembelea Banda la Maonesho la Wizara ya Fedha, ili kupata huduma zinazotolewa na Wizara kupitia Wizara yenyewe na Taasisi zilizochini yake, hatua inayolenga kuimarisha uwazi na uwajibikaji kati ya Wizara na wananchi.

Maonesho ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) yanafanyika katika Viwanja vya Mwl. J.K Nyerere, jijini Dar es Salaam, kuanzia Juni 28 hadi Julai 13, 2026, yakiwa na Kaulimbiu kuu "Maonesho ya Biashara ya Kimataifa Sabasaba ni Fahari ya Tanzania" ikiwa ni sambamba na kuadhimisha miaka 50 tangu kuanzishwa kwa Maonesho hayo.

Lengo kuu la ushiriki wa Wizara na Taasisi zake katika Maonesho hayo ni kusogeza huduma karibu na jamii na kutoa elimu ya kifedha itakayosaidia kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu utekelezaji wa bajeti ya Serikali, usimamizi wa rasilimali za Taifa na fursa na huduma mbalimbali za masomo na kiuchumi zinazopatikana nchini.

Maafisa kutoka Idara na Vitengo mbalimbali vya Wizara ya Fedha na Taasisi zake, wanaoshiriki maadhimisho hayo ni pamoja na Maafisa kutoka Idara ya Bajeti, Idara ya Pensheni, Idara ya Usimamizi wa Sera za Ununuzi wa Umma, Idara ya Uendelezaji Sekta ya Fedha, Idara ya Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu, Idara ya Uchambuzi wa Sera, Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Kitengo cha Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi.

Aidha, katika Banda la Wizara ya Fedha, Watumishi kutoka Taasisi mbalimbali za Wizara hiyo, wanapatikana ili kutoa huduma kwa wananchi na wafanyabishara wote, ikiwemo watumishi kutoka Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA), Mfuko wa uwekezaji wa Utt Amis, Bodi ya Wataalamu wa Ununuzi na Ugavi (PSPTB), Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA), Chuo Cha Usimamizi wa Fedha (IFM), na Soko la Hisa la Dar Es salaam (DSE).

Taasisi nyingine zinazopatikana katika Banda la Wizara ya Fedha ni pamoja na Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA), Chuo Cha Uhasibu Arusha (IAA), Mfuko wa Self (Self Microfinance), Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA), Benki ya Maendeleo (TIB), Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS), Soko la Bidhaa Tanzania (TMX), Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA), Wakala wa Huduma za Ununuzi Serikalini (GPSA), Ofisi ya Usuluhishi wa Malalamiko na Taarifa za Kodi (TOST) pamoja na Chuo Cha Mipango ya Maendeleo Vijijini (IRDP).

Wananchi wote wanakaribishwa kutembelea Banda hilo, ambapo wataalamu waliobobea kutoka Idara na Taasisi mbalimbali zilizo chini ya Wizara wapo tayari kutoa huduma na ufafanuzi wa kina kuhusu masuala ya sera za kodi, bajeti kuu ya Serikali, na pamoja na huduma mbalimbali zinazotolewa na Wizara ya Fedha na taasisi zake.

Mwandishi Mwendesha Ofisi Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Fedha, Bi. Masia Msuya, akiwasainisha kitabu cha wageni wananchi waliotembelea Banda la Wizara ya Fedha, katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), yenye Kaulimbiu kuu "Maonesho ya Biashara ya Kimataifa Sabasaba ni Fahari ya Tanzania", yanayofanyika katika viwanja vya Mwl. J.K Nyerere, jijini Dar es Salaam.

Afisa Mikopo Wa Hazina Saccoss, Bi. Miriam Msalanga, akitoa elimu kuhusu mikopo inayotolewa na chama hicho, kwa wananchi waliotembelea Banda la Wizara ya Fedha katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), yenye Kaulimbiu kuu "Maonesho ya Biashara ya Kimataifa Sabasaba ni Fahari ya Tanzania", yanayofanyika katika viwanja vya Mwl. J.K Nyerere, jijini Dar es Salaam.

Afisa Hesabu, Huduma za Mfuko Mkuu, Wizara ya Fedha, Bi. Juliana Owiso, akitoa maelezo kuhusu uhakiki wa wastaafu, kwa wananchi waliotembelea Banda la Wizara ya Fedha, katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), yenye Kaulimbiu kuu "Maonesho ya Biashara ya Kimataifa Sabasaba ni Fahari ya Tanzania", yanayofanyika katika viwanja vya Mwl. J.K Nyerere, jijini Dar es Salaam.



Maafisa wa Wizara ya Fedha, wakiendelea kutoa elimu kwa wananchi waliotembelea Banda la Wizara ya Fedha katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), yenye Kaulimbiu kuu "Maonesho ya Biashara ya Kimataifa Sabasaba ni Fahari ya Tanzania", yanayofanyika katika viwanja vya Mwl. J.K Nyerere, jijini Dar es Salaam.(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, WF- Dodoma.)


Newala, Mtwara


‎Kukamilika kwa mradi wa ujenzi wa daraja la mawe la Kanyunye na ufunguaji wa barabara yenye urefu wa kilomita 2.6 katika kijiji cha Kanyunye, wilayani Newala kumeleta suluhisho la kudumu la usafiri na usafirishaji wa mazao hususani zao la korosho linalozalishwa kwa wingi katika kijiji hicho.

‎Akizungumza wakati wa ziara ya kutembelea miradi inayotekelezwa na TARURA kupitia mradi wa RISE programu ya kuondoa vikwazo barabarani (Bottleneck), Meneja wa TARURA wilaya ya Newala, Mhandisi Silvester Balama amesema waliibua mradi huo kutokana na changamoto ya mawasiliano ambayo wananchi wa eneo hilo walikuwa wakikabiliana nayo.

‎"Wakazi wa kijiji hiki wengi ni wakulima wa zao la korosho na ghala lao la kihifadhi korosho zikishavunwa lipo katika kijiji cha Moneka kwa hiyo walikuwa wanapata shida kusafirisha mazao yao kutoka Kanyunye kwenda Moneka kwa sababu ya kukosekana kwa kivuko na barabara" ,amesema Mhandisi Balama.

‎Ameongeza kuwa ili mazao yao yaweze kufika katika kijiji cha Moneka ambako ndipo lilipo ghala la kihifadhia korosho ilikuwa lazima wazunguke upande mwingine katika vijiji vya wilaya ya Masasi ili waweze kulifikia ghala hilo.

‎"Uwepo wa kivuko hiki kumesaidia kutoa mazao moja kwa moja kutoka kijiji cha Kanyunye kwenda kijiji cha Moneka ambako kuna ghala lao. Pia kijiji cha Kanyunye hakina shule, shule yao ya msingi ipo kijiji cha Moneka, watoto walikuwa wanapata shida sana namna ya kuvuka kwenye mto huu kwa hiyo baada ya ujenzi huu imekuwa ni ukombozi mkubwa kwao kwa maana sasa watoto wanapita juu na wanawahi kufika shule".

‎Bi. Zainabu Mohamedi Seif mkazi wa kijiji cha Kanyunye amesema kabla ya ujenzi wa daraja hilo walikuwa wakitembea umbali mrefu kuzifikia huduma za afya hospitali ambayo ipo mjini Newala lakini sasa hivi wanakodi bodaboda tu kwenda Newala kwa wakati na kwa gharama nafuu.

‎Kwa upande wake, Bw. Mohamed Seif Hussein maarufu mzee Mchomolo amesema wao kama wananchi wamefurahishwa na ujenzi wa daraja hilo na kwamba limewakomboa kwa namna nyingi.

‎"Hii njia ilikuwa ni ya kichochoro baada ya kutengeneza barabara na kujengwa hili daraja sasa hivi imekuwa barabara maarufu ya kupita sio sisi tu bali hata wenzetu wa kijiji jirani cha Mwanona wameacha kuzunguka huko sasa hivi wanapita barabara hii kwenda Newala, kabla ya hapo tulikuwa tunateseka sana" amesema mzee Mchomola.


Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Chama cha Mapinduzi kutoka Zanzibar wametembelea hifadhi ya Ngorongoro na kustaajabishwa na historia ya binadamu, malikale, Urithi wa Utamaduni na Wanyamapori na kutoa wito kwa watu mbalimbali kutembelea hifadhi hiyo yenye hadhi tatu za Kimataifa zinazotambuliwa na UNESCO

Akizungumza kwa niaba ya wabunge hao mbunge wa viti maalum Mhe. Zainab Abdallah ameeleza kuwa katika ziara hiyo wameshuhudia maendeleo yaliyotukuka kuhusu uhifadhi, utalii, Malikale, urithi wa utamaduni na maendeleo ya jamii ambapo vinadhihirisha kuwa Ngorongoro ni kivutio bora cha Utalii Barani Afrika.

“Kuona ni kuamini, jana na leo tumetembelea eneo la hifadhi ya Ngorongoro na tumeona maendeleo makubwa yakifanyika na kwa macho yetu tumeshuhudia idadi kubwa ya watalii waliojawa na nyuso za bashasha na furaha kwa kushuhudia vivutio vilivyopo, mandhari na hali ya hewa ambayo unaipata Ngorongoro pekee”,amesema Mhe. Zainab.

Wabunge katika ziara hiyo walielezwa kuhusiana na historia ya kutokea kwa kreta ya Ngorongoro, chimboko la binadamu wa kale na namna ambavyo mabadiliko ya viumbe mbalimbali yanavyoendelea kutokea kwa nyakati tofauti.

Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi anayesimamia Idara ya maendeleo ya jamii, Gloria Bideberi akizungumza kwa niaba ya kamishna wa Uhifadhi Ngorongoro, Abdul-Razaq Badru amewapongeza wabunge hao kwa kufanya maamuzi sahihi ya kutembelea hifadhi hiyo yenye vivutio mbalimbali na kuwaomba kuendelea kuwa mabalozi wa kuitangaza Ngorongoro ambayo imepata tuzo ya kuwa chaguo la Wasafiri(Watalii) la kiwango cha Juu cha Ubora mwaka 2026 (Travellers Choice Awards, Best of the best 2026)

Eneo la hifadhi ya Ngorongoro linasifika duniani kutokana na kuwa na ikolojia yenye mchanganyiko wa viumbe mbalimbali kuishi kwa pamoja Ngorongoro kwa miaka mingi.













Top News