Na Karama Kenyunko - Michuzi Tv

TUME ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU) imefungua rasmi dirisha la maombi ya udahili kwa waombaji wa Shahada ya Kwanza kwa mwaka wa masomo 2026/2027, huku ikiwataka waombaji kufuata taratibu rasmi na kujiepusha na matapeli wanaojifanya mawakala wa udahili.

Dirisha hilo limefunguliwa leo Julai 10, 2026 na litabaki wazi hadi Agosti 10, 2026, ambapo waombaji wote wenye sifa wanatakiwa kuwasilisha maombi yao moja kwa moja kwenye vyuo walivyochagua kupitia mifumo ya kielektroniki ya vyuo husika.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Julai 10, 2026 Katibu Mtendaji wa TCU, Profesa Charles Kihampa, amesema makundi yanayostahili kuomba udahili ni wenye sifa za Kidato cha Sita, wenye Stashahada (Diploma) au sifa linganifu, pamoja na wenye Cheti cha Awali (Foundation Certificate) kutoka Chuo Kikuu Huria cha Tanzania.

Kihampa amesema waombaji wanapaswa kusoma kwa makini Mwongozo wa Udahili wa Shahada ya Kwanza wa mwaka 2026/2027 unaopatikana katika tovuti ya TCU ili kujua sifa za kujiunga, programu zinazotolewa na vyuo vilivyoidhinishwa pamoja na masharti mengine ya udahili.

Aidha, waombaji wametakiwa kutembelea tovuti za vyuo wanavyotarajia kujiunga navyo ili kupata maelezo ya kina kuhusu programu za masomo, vigezo vya udahili na namna ya kutuma maombi.

Waombaji watanzania wenye vyeti vilivyotolewa nje ya nchi, TCU imeelekeza kuwa ni lazima wapate ithibati ya ulinganifu wa vyeti vyao kutoka Baraza la Mitihani la Tanzania (NECTA) kwa vyeti vya elimu ya sekondari au Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (NACTVET) kwa vyeti vya stashahada kabla ya kutuma maombi.

Kwa upande wa waombaji wasiokuwa Watanzania wenye vyeti vya nje, wameelekezwa kuwasilisha maombi yao moja kwa moja kupitia mifumo ya vyuo husika.

Aidha Kihampa amewahimiza waombaji kuendelea kupata taarifa sahihi kupitia tovuti ya Tume, tovuti za vyuo vinavyodahili wanafunzi wa Shahada ya Kwanza na kupitia taarifa rasmi zinazotolewa na Tume.

Wakati huo huo, Tume imetoa tahadhari kwa waombaji na wananchi kwa ujumla kujihadhari na matapeli wanaojitambulisha kuwa mawakala au washauri wa udahili, ikisisitiza kuwa huduma zote za udahili zinapatikana moja kwa moja kupitia vyuo husika.

TCU imeeleza kuwa waombaji wanaohitaji ufafanuzi kuhusu udahili wanapaswa kuwasiliana moja kwa moja na vyuo walivyochagua, huku maswali ya jumla yakitumwa kupitia barua pepe ya Tume.



Katibu wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa, Mambo ya Siasa na Uhusiano wa Kimataifa (SUKI) Ndugu Rabia Abdalla Hamid, ametembelea wanufaika wa mikopo ya halmashauri kwa makundi maalum mkoa wa Mbeya.

Akizungumza alipotembelea na kukagua miradi hiyo wakati wa kusikiliza makundi ya kijamii Mkoa wa Mbeya, Rabia aliwataka wanufaika wa mikopo hiyo kurejesha kwa wakati ili kuweza kuendelea kunufaisha na wengine.

"Nimeridhishwa na vikundi hivi vya Samaki na kiwanda kidogo cha Fanicha, ni miradi mizuri na inamanufaa kwa wanufaika wa Mikopo hii na jamii kwa ujumla. Inaridhisha na ina onyesha uwezako mkubwa wakurejesha ," alisema.

Aidha ndugu Rabia amesema Serikali chini ya Dkt Samia Suluhu Hassan itaendelea kutatua na kuhakikisha upatikanaji wa Mikopo kwa makundi yote stahiki, amezitaka Halmashauri kuendelea kuongeza Kasi ya Utoaji wa mikopo hiyo kwa wale wenye sifa stahiki.

















Na. Jacob Kasiri - Arusha.

Uongozi mpya ndani ya Shirika kongwe la uhifadhi nchini umechukua hatamu rasmi baada ya aliyekuwa Kamishna wa Uhifadhi - TANAPA CPA Musa Nassoro Kuji kumaliza muda wake wa uongozi na kukabidhi kijiti hicho kwa Kamishna mpya wa Uhifadhi - TANAPA Massana Mwishawa, makabidhiano yaliyofanyika Julai 08, 2026 Makao Makuu ya Shirika hilo Majengo jijini Arusha.

Kamishna Mwishawa aliteuliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Julai 02, 2026 na jana Julai 09, 2026 Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji alimvika cheo kipya na kumuapisha ili kuliongoza Shirika hilo linalosimamia Hifadhi za Taifa 21 nchini zenye ukubwa wa takribani kilometa za mraba 97,099 ambazo ni sawa na asilimia 10.23 ya eneo lote la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Akizungumza wakati wa hafla ya makabidhiano ya nyaraka na vitendea kazi mbalimbali, Kamishna wa Uhifadhi (Mst.) CPA. Musa Nassoro Kuji alisema;

“Natoa shukrani zangu kwa Mhe. Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuniamini kuliongoza Shirika hili, viongozi wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Bodi ya Wadhamini, watumishi na wadau wote kwa ushirikiano walionipatia katika kipindi chote cha uongozi wangu kwani mafanikio yote yaliyopatikana yametokana na mshikamano, weledi na kujituma kwa pamoja.”

Aidha, Kamishna Kuji aliongeza, “Lenye mwanzo halikosi kuwa na mwisho, ninastaafu utumishi wa umma nikiwa na furaha ya kuona mengi tumeyafikia kwa umoja wetu, niko tayari kutoa ushauri na mchango wangu kila mtakapouhitaji kwani mafanikio ya TANAPA yataendelea kuwa fahari yangu.”

Kwa upande wake Kamishna wa Uhifadhi - TANAPA Massana Mwishawa alisema kuwa majukumu ya taasisi anayokabidhili leo ni dhamana kubwa, alimuhakikishia mtangulizi wake na watanzania kuwa ataifanya kwa uaminifu na uadilifu mkubwa ili shirika hilo lifikie adhma ya serikali ya watalii milioni nane ifikapo 2030.

Kamishna Mwishawa aliongeza, “Kuaminiwa na kupewa jukumu hili na Mhe. Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kiasi kikubwa umetokana na mchango wa mapendekezo yako, hivyo nikuahidi kuendeleza misingi ile ulioiacha ya uwazi, uwajibikaji na ubunifu katika kuiongoza TANAPA”.

Sambamba na hilo Kamishna Mwishawa aliwataka maafisa na askari wote kuendeleza utamaduni wa TANAPA wa kushirikiana, kutoa ushauri na mapendekezo panapohitajika ili kufikia malengo ya Taasisi.

Kamisha Mwishawa ni mbobezi katika nyanja za Uhifadhi, ulinzi mkakati wa maliasili na utalii na ana Shahada ya Uzamili katika Masuala ya Usimamizi wa Maliasili, kabla ya uteuzi wake Julai 02, 2026 alikuwa ni Naibu Kamishna wa Uhifadhi na Maendeleo ya Biashara nafasi aliyoitumikia kuanzia Aprili 29, 2024 baada ya kuteuliwa na Bodi ya Wadhamini - TANAPA.

Vilevile, Kamishna Mwishawa ameshika nyadhifa mbalimbali katika Shirika hilo ikiwemo Meneja wa Ulinzi - TANAPA Makao Makuu (2015 - 2019), Mkuu wa Kanda ya Mashariki, Mkuu wa Hifadhi za Taifa Serengeti na Kisiwa cha Rubondo, pia alihudumu kama Mkuu wa Kitengo cha Himasheria - Hifadhi ya Taifa Kilimanjaro.












Na. Mwandishi wetu, DODOMA

Meneja wa Kanda Namba Sita, Lucas Nkelege amefungua rasmi kikao cha kwanza cha watumishi wa kanda kwa mwaka wa fedha 2026/2027, kilichofanyika kwa lengo la kuweka mwelekeo wa utekelezaji wa majukumu na vipaumbele vya taasisi katika mwaka mpya wa fedha.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao hicho, aliwataka watumishi kufanya kazi kwa weledi, uwajibikaji na ushirikiano ili kufanikisha malengo ya taasisi.

"Mwaka mpya wa fedha unapaswa kuwa mwanzo wa kuongeza ubunifu, uwajibikaji na ushirikiano katika utekelezaji wa majukumu yetu. Kila mtumishi ana wajibu wa kuhakikisha anatimiza majukumu yake kwa ufanisi na kutoa huduma bora zinazokidhi matarajio ya wananchi na wadau wetu," alisema Nkelege.

Aidha, aliwahimiza watumishi kuzingatia maadili ya utumishi wa umma, kufuata sheria, kanuni na taratibu za kazi, pamoja na kushirikiana katika kutekeleza mipango iliyowekwa kwa mwaka wa fedha 2026/2027.

Kikao hicho kilitoa fursa kwa watumishi kujadili vipaumbele vya mwaka mpya wa fedha, kuweka mikakati ya utekelezaji wa shughuli mbalimbali na kuimarisha ushirikiano ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma.






Tanzania imepata heshima ya kutunukiwa Tuzo ya Kimataifa ya WSIS Prizes 2026 kutokana na mafanikio ya utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa minara 758 ya mawasiliano ulioongeza upatikanaji wa huduma za mawasiliano katika maeneo ya vijijini na ambayo hayakuwa na huduma ya mawasiliano nchini.

Tuzo hiyo imepokelewa na Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki(Mb.) katika hafla iliyofanyika Geneva, Uswisi, ikiwa ni utambuzi wa mafanikio ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuimarisha miundombinu ya mawasiliano. Mradi huo ulizinduliwa rasmi na Mhe. Rais tarehe 10 Aprili, 2026.

Mbali na kutwaa tuzo hiyo, Tanzania ilipata uteuzi katika vipengele saba (7) vya Tuzo za WSIS 2026 na kufanikiwa kuibuka na tuzo mbili kwa ujumla, huku pia ikitunukiwa vyeti vya kutambua miradi iliyofanya vizuri.




NA DENIS MLOWE, IRINGA


MCHEZAJI wa Yanga SC na Timu ya Taifa ya Tanzania, Clement Mzize, ametangaza rasmi kufanyika kwa tamasha la hisani la "Washike Mkono" litakalofanyika Julai 12 katika Uwanja wa Samora mkoani Iringa, likiwa na lengo la kukusanya fedha za kusaidia makundi yenye mahitaji maalumu pamoja na kuhamasisha mshikamano kupitia michezo na burudani.

Akizungumza na waandishi wa habari, Mzize alisema tamasha hilo ni mwendelezo wa juhudi zake za kurudisha kwa jamii kile alichojaliwa, huku akisisitiza kuwa kaulimbiu ya "Washike Mkono" inalenga kuwafikia wananchi wenye uhitaji kupitia sekta mbalimbali.

Alisema katika tamasha hilo bodaboda 100 watanufaika kwa kupewa mafuta, helmeti na reflector, huku msaada mwingine ukielekezwa kwenye shule kwa kujenga vyoo na hospitali kwa kutoa vifaa vya tiba ikiwemo mashine ya ultrasound.

Mzize aliwashukuru wadhamini mbalimbali waliowezesha maandalizi ya tamasha hilo, akiwemo GSM, Asas, Master Lim, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Jeshi la Polisi pamoja na wadau wengine waliotoa ushirikiano.

Alisema tiketi ya kuingia ni shilingi 3,000 pekee na kwamba kila tiketi itanunuliwa ni mchango wa moja kwa moja kwa ajili ya kuwasaidia watu wenye mahitaji.

"Tunawaomba wana Iringa na Watanzania kwa ujumla wajitokeze kwa wingi ukitoa shilingi 3,000 unakuwa sehemu ya kuwashika mkono wale wenye uhitaji lengo letu si burudani pekee bali kugusa maisha ya watu," alisema Mzize.

Mzize alisema kuwa mbali na mchezo wa hisani, tamasha hilo litakuwa na burudani mbalimbali zikiwemo muziki wa wasanii, michezo ya watoto, mechi za veterani pamoja na fursa kwa mashabiki kupiga picha na nyota wa soka watakaoshiriki.

Mzize alisema mastaa kadhaa wa soka wamethibitisha kushiriki, akiwemo Feisal Salum, Maxi Nzengeli, Bakari Mwamnyeto, Denis Nkane, Kibwana Shomari, Lomalisa Mutambala pamoja na wachezaji wengine wengi wa ndani na nje ya nchi.

Kwa upande wake, mchezaji Oscar Evaristo anayekipiga katika klabu ya Port Fouad ya nchini Misri alisema amefurahia kushirikiana na Mzize katika tamasha hilo kwa lengo la kuwasaidia wenye mahitaji na wakati huohuo kutoa nafasi kwa vipaji vya soka vya Iringa kuonekana.

Oscar alisema kikosi chake kitakuwa na nyota mbalimbali ambao hakutaka kuwataja wote mapema ili kutoa nafasi ya mashabiki kupata mshangao siku ya tamasha, huku akibainisha kuwa baadhi ya wachezaji wa Iringa watapewa nafasi ya kuonyesha uwezo wao mbele ya wadau wa soka.

Naye Afisa Utamaduni na Michezo Mkoa wa Iringa, Steven Sanga, alisema Ofisi ya Mkuu wa Mkoa imekuwa ikishirikiana kwa karibu na Mzize Foundation kuhakikisha maandalizi yote yanakamilika kwa wakati.

Alisema maandalizi muhimu yamekamilika, ikiwemo upatikanaji wa uwanja, huduma za kwanza, uratibu wa utoaji damu na ushirikiano wa taasisi mbalimbali za serikali ngazi ya mkoa na wilaya.

Sanga alibainisha kuwa tamasha hilo litakuwa zaidi ya mchezo wa soka kwa kuwa litatoa fursa ya burudani, kujifunza kutoka kwa wachezaji wa kiwango cha juu na kuimarisha mshikamano wa wananchi kupitia michezo.

Mgeni rasmi katika tamasha hilo anatarajiwa kuwa Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Kheri James huku waandaaji wakitoa wito kwa wananchi kujitokeza kwa wingi kushuhudia burudani na wakati huohuo kuchangia kuwasaidia watu wenye mahitaji kupitia tamasha la "Washike Mkono".






Mbunge wa jimbo la Kilindi mkoani Tanga Salehe Mbwana Mhando akiendelea kuwafikia Wananchi wa maeneo mbalimbali moja kwa moja hivi karibuni, pichani (mwenye koti) Mhe.Salehe akiwa katika kata ya Mkindi ndani ya jimbo hilo akijumuika na Wananchi kwa mazungumzo ikiwemo kusikiliza changamoto zao na kuzitafutia ufumbuzi.













Serikali imeahidi kuendelea kuwaunga mkono wazalishaji wa ndani ili kuongeza uwezo wa uzalishaji na kukuza mauzo ya bidhaa nje ya nchi hatua inayolenga kuimarisha uchumi wa viwanda na kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania katika masoko ya kimataifa.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Judith Kapinga(Mb), Julai 09, 2026 wakati akizungumza na Waandishi wa Habari baada ya ziara yake katika Kiwanda cha Kamal Refinery kilichopo Bagamoyo mkoani Pwani kinachojihusisha na uchakataji wa mafuta machafu ya mitambo na magari (Waste/Used Lube Oil) ili kuyasafisha na kuzalisha mafuta mapya ya vilainishi (lubricants) na mafuta mazito ya viwandani (heavy fuel oil).

Aidha, amesema Sekta ya Viwanda na Biashara imeweka kipaumbele cha juu katika kuongeza minyororo ya thamani ya uzalishaji hapa nchini mkakati unaolenga kupunguza utegemezi na uingizaji wa bidhaa kutoka nje ambazo zina uwezo na sifa ya kuzalishwa kikamilifu na viwanda vya ndani.

Amesema uwekezaji huo umebainika kuwa na manufaa makubwa kimazingira, kwani unachangia kuweka mazingira katika hali ya usafi na usalama katika wakati ambao Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, akiwa kinara na “Champion” wa utunzaji wa mazingira.

Aidha, amesema ili kufanikisha azma hiyo, Sekta ya Viwanda na Biashara itashirikiana kwa karibu na Wizara yenye dhamana ya Mazingira, ambayo tayari ina uhusiano wa kikazi na kiwanda hicho ili kuhakikisha kiwanda hicho kinaongeza uzalishaji na kukuza biashara huku kikizingatia kikamilifu utunzaji endelevu wa ikolojia.

Vilevile, Amewasihi wadau mbalimbali kuunga mkono kiwanda hicho, kinachosaidia kulinda mazingira ya taifa kwa vizazi vijavyo huku akiwataka Watanzania kuendelea kuchangamkia fursa za kiuchumi zinazojitokeza.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Kiwanda hicho Bw. Sameer Santosh ametoa shukrani za dhati kwa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuweka mazingira wezeshi ya biashara na kuwaunga mkono wazalishaji wa ndani.

Amesema kiwanda hocho kitaendelea kuongeza zaidi uwezo wa uzalishaji ili kupunguza uingizaji wa bidhaa hizo kutoka nje ya nchi.

Top News