Na Mwandishi Wetu, Arusha.

Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela kwa kushirikiana na Taasisi ya Global Education Link Ltd wamesaini hati ya makubaliano ya ushirikiano yenye lengo la kukuza tafiti, ubunifu na maendeleo ya kisayansi.

Makubaliano hayo yatakayosaidia kuandaa kizazi kipya kitakacholeta mapinduzi ya kiuchumi na kiteknolojia Barani Afrika na duniani kwa ujumla.

Ushirikiano huo unatarajiwa kufungua milango ya fursa mpya katika sekta ya elimu, utafiti na ubunifu, pamoja na kuitangaza taasisi hiyo kimataifa ili dunia itambue kuwa Tanzania ina taasisi inayozalisha vipaji na teknolojia za kisasa kupitia ushirikiano na vyuo vikuu mbalimbali vya nje ya nchi.

Akizungumza mara baada ya kusainiwa kwa makubaliano hayo, Makamu Mkuu wa Taasisi ya Nelson Mandela, Profesa Maulilio Kipanyula, alisema Afrika ina hazina kubwa ya vipaji ambavyo vikisimamiwa na kupangwa vizuri vinaweza kutoa suluhisho la changamoto mbalimbali zinazoikabili jamii.

Profesa Kipanyula alisisitiza kuwa ubunifu na maendeleo ya kisayansi hayawezi kufikiwa bila ushirikiano wa taasisi mbalimbali, akibainisha kuwa makubaliano hayo ni hatua muhimu katika kuongeza idadi ya wanafunzi, hususan wanafunzi wa kimataifa, pamoja na kuchangia kukuza uchumi.

Alisema makubaliano hayo ni ya kimkakati katika kuhakikisha elimu inayotolewa inaendelea kuimarika kimataifa kwa kuvutia vipaji vya vijana kusoma na kuwasilisha bunifu zao kupitia Taasisi ya Nelson Mandela.

Aidha, alieleza kuwa anatamani kuona taasisi hiyo ikiendelea kuzalisha na kulea vipaji vya vijana pamoja na ubunifu mbalimbali utakaosaidia kuchochea maendeleo katika majukwaa ya kitaifa na kimataifa.

“Tunataka tafiti zetu na matokeo yake yawafikie wananchi kwa haraka zaidi, ambapo ubunifu na maarifa vitakuwa na mchango mkubwa kwa jamii. Utafiti na ubunifu lazima viwe na uwezo wa kutatua changamoto za watu,” alisema Profesa Kipanyula.

Naye Mkurugenzi wa Taasisi ya Global Education Link Ltd, Abdullmalik Mollel, alisema ushirikiano huo umejikita katika kuimarisha masuala ya kitaaluma, uwekezaji na matumizi ya teknolojia ili kuongeza tija katika sekta ya elimu na uchumi.

Alisema elimu inayotolewa kwa wanafunzi inapaswa kuwa na mchango wa moja kwa moja katika kukuza uchumi na maendeleo kwa kutumia teknolojia, maarifa na mitaji.

“Elimu anayopewa mwanafunzi inapaswa kusaidia kukuza uchumi na kuleta maendeleo kupitia teknolojia, maarifa na uwekezaji. Ushirikiano wa maarifa kati ya vyuo vikuu mbalimbali utaongeza tija katika kukuza uchumi unaotegemea teknolojia,” alisema Mollel.

Aliongeza kuwa makubaliano hayo ni mwanzo wa safari ya ushirikiano wa muda mrefu kati ya taasisi hizo mbili, wenye lengo la kuimarisha ushirikiano wa vyuo vikuu na kuleta mabadiliko chanya katika sekta ya elimu, utafiti na maendeleo ya jamii kwa ujumla.








Shirika lisilo la kiserikali la Kikristo ECHO East Africa kutoka Ngaramtoni jijini Arusha limefanya warsha ya mafunzo kwa vitendo kwa waandishi wa habari kutoka vyombo mbalimbali vya habari jijini Arusha kuhusu Kilimo Ikolojia (Agroecology).

Shirika hilo linafanya kazi katika nchi za Afrika Mashariki pamoja na baadhi ya nchi za Kusini mwa Afrika, Lengo ni kuwasaidia wakulima, hususan wakulima wadogo, kwa kuwapatia mbinu mbadala, elimu, ujuzi na maarifa ili kuongeza uzalishaji wa mazao yao kwa kutumia mbinu rafiki kwa mazingira, ikiwemo kilimo ikolojia.

Warsha hiyo ya mafunzo kwa vitendo imefanyika kwa siku mbili na Dhumuni la mafunzo hayo ni kuwaleta pamoja waandishi wa habari kutoka vyombo mbalimbali ili kuwafahamisha juu ya uwepo wa shirika hilo, kuelewa shughuli mbalimbali zinazotekelezwa, pamoja na kuwapa elimu kuhusu kilimo ikolojia.

Katika mafunzo hayo, waandishi wa habari wamepata fursa ya kufanya ziara katika maeneo mbalimbali ndani ya shirika hilo na kujifunza masuala kadhaa ya kilimo ikolojia. Miongoni mwa mambo waliyojifunza ni pamoja na mbinu za uvunaji wa maji ili kupunguza mmomonyoko wa udongo, kilimo mseto, upandaji wa miti, na matumizi ya mazao yanayofunika ardhi ili kulinda rutuba ya udongo.

Aidha, washiriki wametembelea miradi mbalimbali inayotekelezwa na shirika hilo, ikiwemo benki ya mbegu, uzalishaji wa biogas, matumizi ya mitambo ya kukaushia vyakula, pamoja na kutembelea wakulima ambao ni wanufaika wa mbinu za kilimo ikolojia.

Kilimo Ikolojia (Agroecology) ni mfumo wa kilimo unaochanganya kanuni za ikolojia, yaani mazingira ya asili, na uzalishaji wa mazao. Lengo lake ni kuzalisha chakula kwa njia rafiki kwa mazingira, endelevu na yenye kunufaisha wakulima pamoja na jamii kwa muda mrefu.

Wataalamu wa kilimo wanaendelea kuhamasisha matumizi ya kilimo ikolojia kama njia mbadala ya kuongeza uzalishaji wa chakula huku wakilinda mazingira. Mbinu hii inahusisha matumizi ya rasilimali za asili, kupanda mazao mchanganyiko, pamoja na kupunguza utegemezi wa kemikali shambani.







-Vodacom Tanzania Foundation Imejenga matundu 10 ya vyoo Shule ya Msingi Mkata

Vodacom Tanzania Foundation kwa kushirikiana na Twende Butiama pamoja na Stanbic Bank wamejenga matundu 10 ya kisasa ya vyoo katika Shule ya Msingi Mkata iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Handeni mkoani Tanga, ikiwa ni sehemu ya kurudisha kwa jamii.

Akipokea matundu hayo 10 ya vyoo kutoka kwa Meneja Mauzo Mwandamizi wa Vodacom Tanzania Kanda ya Kaskazini, Andrew Temu, kwa niaba ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Handeni, Yibarila Chiza alisema vyoo hivyo vitasaidia kulinda afya za wanafunzi pamoja na kuwafanya kuwa mabalozi wa kuhamasisha matumizi ya vyoo bora na vya kisasa majumbani mwao.

Aidha alisema kuwa vyoo hivyo vitachochea ufaulu wa wanafunzi kwa kupunguza changamoto ya uhaba wa matundu ya vyoo katika shule hiyo, na hivyo kuwawezesha wanafunzi kupata mazingira bora ya kujifunzia. Alitoa shukrani kwa wadau hao kwa msaada huo walioutoa kwa shule hiyo.

Kwa upande wake, Meneja Mauzo Mwandamizi wa Vodacom Tanzania Kanda ya Kaskazini, Andrew Temu, alisema Vodacom Tanzania Foundation inaangazia maeneo matatu makuu ambayo ni afya, mazingira na elimu.

Alisema ili mwanafunzi aweze kusoma vizuri anahitaji kuwa katika mazingira rafiki yasiyokuwa na msongo wa mawazo, hivyo ujenzi wa vyoo hivyo utasaidia wanafunzi hasa wenye mahitaji maalum na kuwapa muda zaidi wa kukaa darasani badala ya kupoteza muda kusubiri foleni ya huduma ya choo.

Naye Mwenyekiti wa msafara wa Twende Butiama, Gabriel Landa, alisema wao kama Twende Butiama wameamua kutumia baiskeli kama njia ya kumuenzi Baba wa Taifa kwa kuhamasisha wananchi kuboresha sekta za afya, elimu na mazingira kupitia programu mbalimbali za uhamasishaji.

Awali akitoa taarifa ya shule, Mwalimu Mkuu Msaidizi wa Shule ya Msingi Mkata, Daliana Majatta, alisema matundu hayo ya vyoo yamesaidia kupunguza uhitaji wa vyoo katika shule hiyo, ingawa bado wanahitaji jumla ya matundu 28 ili kukidhi mahitaji yaliyopo.

"Pamoja na mafanikio hayo, shule yetu bado ina changamoto mbalimbali zinazoifanya isiwe ya kisasa zaidi, ikiwemo miundombinu ya madarasa kwa ajili ya wanafunzi wenye mahitaji maalum pamoja na upungufu wa madawati 300, wakati idadi ya wanafunzi ni 2,023," alisema Majatta.

Mbali na ujenzi wa matundu hayo 10 ya vyoo, Vodacom Tanzania Foundation pia imewahi kutoa misaada mbalimbali katika shule hiyo ikiwemo viti mwendo kwa wanafunzi wenye mahitaji maalum, magodoro, vitanda pamoja na mashuka.
Meneja Mauzo Mwandamizi wa Vodacom Tanzania Kanda ya Kaskazini, Andrew Temu, akizungumza wakati wa makabidhiano ya matundu 10 ya vyoo vya kisasa vilivyojengwa na Vodacom Tanzania Foundation katika Shule ya Msingi Mkata iliyopo wilayani Handeni mkoani Tanga. Ujenzi wa vyoo hivyo unalenga kutimiza dhamira ya Vodacom ya kuchangia kuboresha mazingira ya kujifunzia kwa wanafunzi wote, huku ikiangazia afya na ustawi wa wanafunzi kupitia miradi ya maendeleo ya jamii. Tukio hilo lililofanyika jana lilihudhuriwa na Yibarila chiza, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji Wilaya ya Handeni (kulia), Meneja Uhusiano wa masuala ya serikali wa Vodacom Tanzania Grace Lyon (Kushoto), Mwenyekiti wa Msafara wa Twende Butiama Gabriel Landa (Wa pili kushoto) pamoja na wazazi, walimu na wanafunzi wa shule hiyo.
Uongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Handeni, Timu ya Vodacom, Wawakilishi wa Twende Butiama na Walimu wakiwa kwenye picha ya pamoja baada ya kufunguliwa kwa vyoo vipya vya kisasa vilivyotolewa na Kampuni ya Mawasiliano na teknolojia ya Vodacom Tanzania Plc katika Shule ya Msingi Mkata, iliyoko wilaya ya Handeni mkoani Tanga.

Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Handeni, Bw Yibarila Chiza na Meneja Mauzo Mwandamizi wa Vodacom Tanzania Plc Kanda ya Kaskazini, Andrew Temu wakikata utepe ikiwa ni ishara ya kufungua rasmi vyoo vya kisasa 10 vilivyojengwa na Kampuni hiyo katika shule ya Msingi Mkata wilayani Handeni mkoani Tanga, Vodacom imetimiza ahadi iliyotolewa kwa shule hiyo wakati wa msafara wa waendesha baiskeli wa 'Twende Butiama' uliopita shuleni hapo mwaka jana ikiwa ni ishara ya kumuenzi Baba wa Taifa Mwl JK Nyerere. Tukio Hilo lilifanyika jumatatu wiki hii mjini Mkata.

Baadhi ya Wanafunzi wa Shule ya Msingi Mkata iliyopo wilayani Handeni Mkoani Tanga, wakifurahia uwepo wa vyoo vipya na vya kisasa 10, vilivyotolewa na Kampuni ya Mawasiliano na Teknolojia ya Vodacom Tanzania. Vyoo hivi vinalenga kuboresha mazingira ya kujisomea ya wanafunzi hao.

Na: Dkt. Reubeni Lumbagala, Tanga

Watoto wana haki zao za msingi. Wanapaswa kupendwa, kulindwa, kusikiliza, kupewa malezi na matunzo. Pia, watoto wanapaswa kupewa mahitaji yote ya msingi yaani chakula, mavazi na malazi. Kimsingi, ni wajibu wa msingi kwa wazazi na walezi hukakikisha watoto wanapata haki na mahitaji yao muhimu ili waweze kufurahia maisha kwa kuzingatia kuwa watoto ni kiungo muhimu katika familia na maendeleo ya Taifa.

Serikali kama mdau muhimu wa ustawi na maendeleo ya watoto, inawajibika kuweka mazingira mazuri ya ustawi wa watoto. Aidha, serikali inawajibika kutunga sheria zitakazowalinda watoto ili kesho zao ziweze kutimia na Taifa linufaike kupitia uwepo wao. Ipo changamoto katika jamii zetu kwa baadhi ya wanawake kutupa watoto pindi wanapojifungua watoto hao. 

Wengine huwatupa katika mazingira ambayo ni rahisi kuokotwa na wapita njia lakini baadhi yao huwatupa katika mazingira mabaya mathalani jalalani ambapo kwa bahati mbaya wengine huokotwa wakiwa tayari wameshapoteza maisha. Mbaya sana.

Kwa sababu yeyote ile, suala la kutupa mtoto si suala zuri hasa mtoto anapotupwa katika mazingira mabaya ambayo yanazalisha matatizo mengine mathalani magonjwa kutokana na kupigwa baridi kali na wengine kupoteza maisha kabisa.

 Zipo sababu kadhaa zikiwemo suala la hali ngumu za maisha au baba mzazi wa mtoto kukataa mimba au kumlea mtoto, na hivyo mwanamke kuamua kumtupa mtoto wake aliyehangaika nae kwa miezi tisa tumboni na uchungu wa kumzaa hospitalini.

Januari 17, 2026, karibu na nyumba ya wageni (Guest House) ijulikanayo kwa jina la Kasulu, Nzega Mjini mkoani Tabora, alitelekezwa mtoto ambapo Ofisi ya Mkuu wa wilaya ya Nzega chini ya uongozi wa Mkuu wa wilaya hiyo, Naitapwaki Tukai pamoja na Jeshi la Polisi wilaya ya Nzega waliamua kumchukua mtoto huyo na kumpeleka hospitali kwa uchunguzi na uangalizi huku jitihada za kumpata mama mzazi wa mtoto huyo zikiendelea.

Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kwa upendo mkubwa alionao kwa watoto na jamii, ameamua kumchukua mtoto huyo ambaye amepewa jina la Grace Samia Suluhu Hassan. Tukio hilo la upendo limefanyika Machi 11, 2026, katika makazi yake ya Ikulu ya Chamwino Jijini Dodoma. Kipekee kabisa, nimpongeze Rais Dk. Samia kwa moyo wake wa upendo kwa mtoto huyo kwa kuamua kuchukua jukumu la kumuasili awe ni sehemu ya watoto na familia yake kimalezi na kimatunzo.

Rais Dk. Samia anatoa matumaini mapya juu ya hatma ya mtoto huyo kuwa yupo kwenye mikono salama na Mwenyezi Mungu amjalie mtoto huyo afya njema ili akue vizuri. "Wanaotupa watoto hawajui wanalolifanya. Kuliko kumtupa mtoto ni afadhali ukamkabidhi katika mamlaka za kisheria au kituo cha kulelea watoto. Kila mtoto aliyezaliwa ni hazina na hatujui kesho yake," amesisitiza Rais Dk . Samia.

Pengine ni muda muafaka kwa wanaume kutimiza majukumu ya kimalezi badala ya kutelekeza familia, na hivyo kuwaachia wanawake njia panda, hali inayosababisha baadhi ya wanawake kufikia hatua ya kuwatupa watoto. 

Lakini jambo la muhimu ambalo Rais Dk. Samia amelisisitiza ni kutumia vituo vya watoto kuomba msaada ya kulelewa mtoto badala ya kumtupa mtoto, jambo ambalo si zuri hata mbele za Mungu na hata katika maadili yetu ya Kitanzania. Kwa hakika, Rais Dk. Samia ameonyesha upendo wa kipekee kwa jamii kwa kumuasili mtoto Grace Samia Suluhu Hassan. Tumuombee mtoto Grace Samia Suluhu Hassan awe na afya njema na siku moja aje kuwa nguzo muhimu kwa nchi yetu ya Tanzania.

Dk. Reubeni Lumbagala ni Mwalimu katika Shule ya Sekondari Funguni ya wilayani Pangani mkoani Tanga.

Maoni : 0620 800 462.







Na MWANDISHI WETU

ZAIDI ya washiriki 600 kutoka ndani na nje ya nchi wanataraji kushiriki semina maalumu ya uendeleaji na upangaji wa miji inayo kua.

Semina hiyo ya siku mbili imeandaliwa na Chama cha Wabunifu Majengo Tanzania (AAT) itafanyika mjini Morogoro kuanzia Aprili 9-10 mwaka huu.

Akizungumza na waandishi wa habari, jijini Dar es Salaam, Rais wa AAT, Meck T’chawi, amesea ni semina muhimu kwani inagusa kwa kiasi kikubwa suala la upangaji miji na ujenzi wa nyumba bora zinazo zingatia teknolojia ya sasa na zamani.

Ameeleza, teknolojia ya ujenzi inakua kwa kasi hivyo kuleta mabadiliko ya ukuaji wa miji.

“Semina hii itasaidia kutoa elimu ya namna ya kupanga miji inayobadilika kuringana na teknolojia ya sasa na ya zamani,”ameeleza T’chawi.

Amebainisha kwa hapa Tanzania miji mingi ilipangwa enzi za ukoloni kipindi cha Mjerumani ingawa changamoto ni kutokana na ongezeko la idadi ya watu linalofanya miji hiyo kuonekana kama skwata.

“Tunahitajika kufanya mbinu mbanndala ili sasa maeneo yanayoonekana ni skwata kuyapanga. Tunaweza kuomba wafadhili li kutusaidia kupanga maeneo hayo. Tukitumia wataalamu wetu inawezekana,”amesema.

Katibu Mtendaji wa AAT, Attie Ahmed Ali, ametoa wito kwa wataalamu wote kushiriki semina hiyo muhimu kwani inawapa wigo mkubwa kutumia ukuaji wa teknolojia na taaluma zao.

“Katika kuunga mkono jitihada za Raisa Dk. Samia Suluhu Hassan katika kukuza sekta ya utalii, semina hii pia itakuwa na tukio la washiriki kwenda kutalii katika mbuga ya wanyama ya Mikumi iliyopo Morogoro,”amesema Attie.

Mwenyekiti wa maandalizi wa semina hiyo, Fortunata Msakamali, alisema washiriki watatoka katika nchi za Afrika Mashariki, Bara la Afrika na dunia kwa ujumla.

“Itashirikisha wabunifu majengo ndani na nje ya jengo, watu wa mandhari, watu wa teknolojia, wasimamizi wa ujenzi, wasimamizi miradi, mipango miji, wahandisi, wakandarasi, waendelezaji majengo, wahadhili na mafundi,”amebainisha.

Mjumbe wa kamati hiyo Catheline Joseph, alisema wakadiriaji wa majenzi wananafasi kubwa kuhakikisha gharama zinazotokana na mabadiliko ya miji zinakuwa sahihi kwaajili ya miji salama ya vizazi vilivyopo na vya baadaye.







Na Said Mwishehe,Michuzi TV-Njombe

WAKALA wa Nishati Vijijini (REA) umetoa rai kwa sekta binafsi nchini kuchangamkia fursa ya kuwekeza katika miradi midogo ya kuzalisha umeme vijijini kwani wakala huo upo tayari kushirikiana nao kwa kila hatua.

Rai hiyo imetolewa leo Machi 11,2026 na Kaimu Meneja Usaidizi wa Kiufundi kwa Waendelezaji wa Miradi kutoka REA, Mhandisi Emmanuel Yessaya mbele ya Wahariri wa vyombo vya habari ambao ni Wanachama wa Jukwaa la Wahariri Tanzania(TEF)walioko katika ziara ya kutembelea miradi inayosimamiwa au kufadhiliwa na wakala huo mkoani Njombe.

Wahariri hao wamepata nafasi ya kuona mradi wa kuzalisha umeme wa kilovati 317 uliopo kwenye Kijiji cha Boimanda katika kata ya Matola wilayani Njombe mkoani Njombe ambapo REA wametoa ruzuku ya Sh.bilioni 5.4 kujenga miundombinu ya mradi huo unaosimamiwa na Shirika la Benedictine Sisters of St. Gertrud Convent

“Miradi ya uzalishaji umeme inayotekelezwa na sekta binafsi ina mchango mkubwa katika kuongeza upatikanaji wa nishati ya uhakika nchini.Hivyo tunaendelea kutoa rai kwa sector binafsi kushiriki katika miradi ya aina hii hasa katika mikoa kama Iringa,Njombe na Ruvuma ambako kuna vyanzo vya maji vinavyoweza kutumika kuzalisha umeme.”

Kuhusu mradi huo wa umeme wa maji Mhandisi Yessaya amesema hadi sasa ujenzi wa miundombinu ya mradi huo umekamilika na kilichobaki ni kuwasha mtambo na kuunganisha umeme katika gridi ya taifa.

Amefafanua kuwa “Mradi huu ulianzishwa kuzalisha umeme kwa matumizi ya shirika ambalo linashughuli mbalimbali zinazohitaji umeme ikiwemo katika hospitali, shule, karakana na gereji.Baadae ulipanuliwa ili kunufaisha jamii kwa kuunganisha vijiji vitatu vya Matola, Boimanda na Kitulila.Hata hivyo REA tulishapeleka umeme katika Vijiji vyote vya Mkoa wa Njombe.”

Wakati huo huo Mratibu wa Mradi wa kuzalisha umeme wa Lupali, Sister Imaculatha Mlowe, amesema REA imechangia kwa kiasi kikubwa kufanikisha kukamilika kwa mradi huo kwani amekuwa Mdau muhimu tangu hatua za awali.

Pia amesema kwa hivi sasa zaidi ya wananchi 212 wa Kijiji cha Boimanda wanapata huduma ya umeme wa TANESCO wakati wananchi 366 wa Kijiji cha Matola wanapata umeme kupitia mradi wa zamani wa Lupali.

Aidha amesema mkataba wa kuuza umeme kati ya TANESCO na Shirika la St. Benedictine of Imiliwaha tayari umeshasainiwa na kazi ya kuanza uzalishaji zinatarajiwa kukamilika ndani ya miezi mitatu ijayo.







 Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amewasihi Viongozi wa dini na Watanzania kwa ujumla kutumia mwezi wa toba wa Ramadhani na Kwaresma kuiombea Nchi, Viongozi wa Serikali na Vyama vya Siasa ili kujenga nchi moja yenye upendo na mshikamano.

Makamu wa Rais, amesema hayo mara baada ya kushiriki Iftari aliyoiandaa kwaajili ya wananchi mbalimbali wa Mkoa wa Dodoma pamoja na Viongozi wa Serikali, Taasisi za Dini na Chama Cha Mapinduzi, iliyofanyika Mkoani Dodoma.

Amesema jambo kubwa ni kuhakikisha hamasa ya mapenzi ya nchi inakuwepo kwa kila mmoja na chemchem ya mapenzi kwa nchi iwepo katika roho ya kila mtanzania ili kuishi kwa kupendana na kushirikiana chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

 Pia, Makamu wa Rais amesema katika mambo ya maana yanayoweza kufanyakika katika mwezi wa toba ni pamoja na kumuahidi Mwenyezi Mungu kwamba kila mtanzania atafanya jitihada ya kuunganisha watanzania kujenga nchi kuwa nchi moja yenye upendo.

Iftar hiyo imehudhuriwa na Viongozi mbalimbali akiwemo Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhandishi Hamad Masauni, Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi Balozi Dkt. Asha-Rose Migiro, Waziri wa Madini Anthony Mavunde, Kamati ya Maridhiano, Viongozi mbalimbali wa Dini, Wabunge wa Mkoa wa Dodoma, Wakuu wa Wilaya pamoja na wananchi.

















-Asisitiza Ushirikiano wa Kimataifa, Majadiliano ya Kimkakati na mbinu za pamoja kukabiliana na changamoto za kidunia.

Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Stephen Mbundi amekutana na Washiriki wa Kozi ya 14 kutoka Chuo cha Taifa cha Ulinzi (NDC) waliotembelea Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mtumba jijini Dodoma kwa ziara ya Mafunzo.

Akizungumza katika kikao na wanachuo hao Mhe. Balozi Mbundi alieleza kufurahishwa kwake na ziara hiyo ambayo inawapatia mafunzo kwa vitendo wanachuo hao na kusisitiza umuhimu wa ushirikiano wa kimataifa, majadiliano ya kimkakati, na mbinu za pamoja kama nyenzo za kukabiliana na changamoto mbalimbali zinazoikabili dunia.

Alisema kuwa mazingira ya usalama duniani yanabadilika kutokana na changamoto mbalimbali kama za mivutano ya kisiasa kati ya mataifa, uhalifu wa kuvuka mipaka, ugaidi, vitisho vya mtandao, mabadiliko ya tabianchi na za kiuchumi.

Aliongeza kuwa ni matumaini yake ziara hiyo itachangia kuimarisha uelewa wa washiriki kuhusu uhusiano kati ya diplomasia, usalama wa taifa na ushirikiano wa kimataifa na kuimarisha ushirikiano kati ya Wizara ya Mambop ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Chuo hicho.

Katika kikao hicho Balozi Mbundi alielezea kwa ufupi historia, majukumu, dira na dhamira ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki katika kusimamia sera ya mambo ya nje, kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia, na kukuza ushirikiano wa kikanda kupitia taasisi kama Jumuiya ya Afrika Mashariki na Umoja wa Afrika.

Naye Mwakilishi wa Mkuu wa Chuo cha NDC, Brigedia Jenerali Selemani Bakari Gwaya alieleza kuridhishwa kwao na mchango wa Wizara katika kufanikisha kozi mbalimbali zinazotolewa na chuo hicho ambao unakiwezesha kukua kimataifa na kuaminika kama taasisi ya kimkakati.

Amepongeza juhudi za Wizara kwa kuendelea kutekeleza diplomasia ya uchumi kwa weledi na Vitendo licha ya changamoto mbalimbali zinazojitokeza katika siasa za kimataifa.

Wanachuo 72 wa Kozi ya 14 ya NDC kutoka nchi 17 za Tanzania, Bangladesh, Botswana, Burundi, Misri, Ethiopia,India, Kenya, Malawi, Namibia, Nigeria, Rwanda, Sierra Leone, Afrika Kusini, Uganda, Zambia na Zimbawe waliambatana na Wakufunzi na Viongozi wao walifika Wizarani kwa lengo la kujifunza jinsi Wizara inavyotekeleza majukumu yake.













Top News