WAZIRI wa Viwanda na Biashara Judith Kapinga, amesema Serikali imeendelea kuweka mazingira bora ya uwekezaji na biashara kwa kuboresha sera, sheria na mifumo ya utoaji huduma kuvutia uwekezaji wenye tija.

Kapinga ameyasema hayo jijini Dar es Salaam wakati wa uzinduzi wa chapa mpya ya magari Jetour, jijini Dar es Salaama, ambapo amefafanua uzinduzi huo unaendana kikamilifu na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Mpango wa Tatu wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano na Ajenda ya Taifa ya Ujenzi wa Uchumi wa Viwanda na Biashara.

Ameongeza uwekezaji huo unadhihirisha dhamira ya kukuza ushiriki wa sekta binafsi, kuongeza matumizi ya rasilimali za ndani,uhamishaji wa teknolojia na kuzalisha ajira kwa Watanzania.

"Tunatambua Africarriers na Jetour hawaleti magari pekee nchini bali wanaleta fursa mpya za biashara, uwekezaji, ajira, maarifa ya kiteknolojia na mchango mkubwa katika maendeleo ya uchumi wa Tanzania na ukanda wetu wa Afrika Mashariki,”amesema Waziri Kapinga.

Pia amewapongeza viongozi wa Africarriers Group na Jetour Global kwa maono yao makubwa kuichagua Tanzania kuwa sehemu ya safari yao ya ukuaji na mafanikio huku akisisitiza Serikali itaendelea kushirikiana na wawekezaji wote wenye nia ya dhati ya kuchangia maendeleo ya Taifa letu.

Akieleza zaidi amesema ujio wa Jetour nchini Tanzania kunafungua ukurasa mpya wa fursa za kiuchumi na uwekezaji huo utazalisha ajira mpya kwa vijana katika maeneo mbalimbali yakiwemo ya mauzo, huduma za kiufundi, ushauri wa huduma kwa wateja, teknolojia ya habari na mawasiliano pamoja na huduma nyingine.

Waziri Kapinga amesema pia mafanikio ya Africarriers kwa kipindi cha zaidi ya miaka 50 ni ushahidi wa uwezo, uthubutu na ustahimilivu wa wafanyabiashara wa Kitanzania.

“Kupitia ushirikiano huo na Jetour, watapiga hatua nyingine muhimu kuelekea Tanzania yenye viwanda imara, ajira nyingi, biashara shindani na uchumi jumuishi kwa kizazi cha sasa na vizazi vijavyo.”

Kwa upande wa Mkuu wa Idara ya Sheria wa Kampuni za Africarries, Ngasa Mboje amesema kwa mara ya kwanza wameleta gari zinazoendana na soko na mahitaji ya Watanzania kwasababu ni gharama nafuu.

“Magari ya Jetour yanauzwa kwa njia ya malipo ya papo kwa hapo na njia ya mpili ni kwa mkopo kwasababu kuna baadhi ya Watanzania hawawezi kumudu gharama kwa mara kwanza.Hivyo unaweza kununua kwa mkopo na kulipa kidogo kidogo, huku ukiendelea kulitumia gari lako.”
Mgeni rasmi Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe.Judidh Salvio Kapinga akizungumza mbele ya Wageni waalikwa mbalimbali waliofika kwenye hafla ya uzinduzi rasmi wa Chapa mpya ya Magari ya Jetour nchini Tanzania,iliofanyika Juni 8,2026 Masaki, jijini Dar es Salaam

Balozi wa Shirikisho la Urusi nchini Tanzania Mhe. Andrey Avetisyuan akizungumza mbele ya Wageni waalikwa mbalimbali waliofika kwenye hafla ya uzinduzi rasmi wa Chapa mpya ya Magari ya Jetour nchini Tanzania,iliofanyika Juni 8,2026 Masaki, jijini Dar es Salaam,ambapo mgeni rasmi alikuwa ni Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe.Judidh Salvio Kapinga
Makamu wa Rais wa Kampuni ya Magari ya Africarriers Group,Bw. Shahid Nabi, akizungumza mbele ya Wageni waalikwa mbalimbali waliofika kwenye hafla ya uzinduzi rasmi wa Chapa mpya ya Magari ya Jetour nchini Tanzania,iliofanyika Juni 8,2026 Masaki, jijini Dar es Salaam,ambapo mgeni rasmi alikuwa ni Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe.Judidh Salvio Kapinga
Baadhi ya Viongozi na wageni waalikwa wakishuhudia uzinduzi wa Chapa mpya ya Magari ya Jetour nchini Tanzania,hafla iliofanyika Juni 8,2026 Masaki, jijini Dar es Salaam.
Mwenyekiti wa Makampuni ya Africarriers, Bw. Fida Rashid, akimkabidhi Balozi wa Jamhuri ya Watu wa China nchini Tanzania, Mhe. Chen Mingjian mfano wa gari ya Jetour iliozinduliwa nchin Tanzania.
Balozi wa Jamhuri ya Watu wa China nchini Tanzania, Mhe. Chen Mingjian akiwasha gari ya Jetour iliozinduliwa nchini Tanzania hapo jana,Masaki jijini Dar es Salaam.
Picha ya pamoja mara baada ya uzinduzi wa Chapa mpya ya Magari ya Jetour nchini Tanzania,hafla iliofanyika Juni 8,2026 Masaki, jijini Dar es Salaam.






Na Janeth Raphael, MichuziTv

Watanzania wanatarajia kupata burudani ya hali ya juu ya soka la kimataifa baada ya Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) kutangaza rasmi kuwa litarusha mubashara Michuano ya Kombe la Dunia la FIFA 2026 bila malipo.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Juni 9, 2026 jijini Dodoma, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TBC, Upendo Mbelle, amesema shirika hilo limefanikiwa kupata haki rasmi za kurusha mashindano hayo makubwa ya dunia yatakayofanyika kuanzia Juni 11 hadi Julai 19, 2026 katika mataifa ya Marekani, Mexico na Canada.

Amesema Watanzania wataweza kufuatilia mashindano hayo kupitia televisheni ya TBC, redio, pamoja na majukwaa ya mtandaoni ikiwemo Facebook, YouTube, Instagram na TikTok, sambamba na tovuti rasmi ya shirika hilo.

“Tumejipanga kuhakikisha Watanzania wanapata matangazo ya ubora wa juu, yakiambatana na uchambuzi wa kina kutoka kwa wachambuzi wenye uzoefu mkubwa wa soka,” amesema Mbelle.

Ameongeza kuwa uzoefu wa muda mrefu wa TBC katika kurusha matukio makubwa ya michezo, tangu enzi za Radio Tanzania Dar es Salaam (RTD), umeiwezesha shirika hilo kuendelea kutoa huduma bora kwa watazamaji na wasikilizaji wake.

Kwa mujibu wa Mbelle, mchezo wa ufunguzi wa Kombe la Dunia 2026 utapigwa Juni 11, 2026, ukiwakutanisha wenyeji Mexico dhidi ya Afrika Kusini, ambapo TBC itakuwa tayari kuurusha mubashara kuanzia dakika ya kwanza.

Aidha, amesema TBC imeweka kaulimbiu maalum ya “Pira Mtelezo”, ikilenga kuwaletea Watanzania burudani ya kipekee ya soka la kimataifa wakiwa majumbani au walipo popote.

Upendo Mbelle amesisitiza kuwa TBC imewahi kurusha pia matoleo ya Kombe la Dunia ya mwaka 2010 Afrika Kusini, 2014 Brazil, 2018 Urusi na 2022 Qatar, jambo linaloonyesha uzoefu wake mkubwa katika utangazaji wa mashindano ya kimataifa.

Pia amebainisha kuwa katika kipindi cha hivi karibuni, TBC imeendelea kuimarisha uwezo wake kupitia kurusha michuano mikubwa kama CHAN 2025 iliyofanyika Tanzania, Kenya na Uganda pamoja na AFCON 2025 iliyofanyika Morocco.

“Tunaendelea kujipanga kuhakikisha kila Mtanzania anapata nafasi ya kushuhudia soka la kiwango cha juu duniani kupitia chombo chake cha habari anachokiamini,” ameongeza.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Masoko wa TBC, Daphrosa Kimbory, amesema shirika hilo limejipanga kikamilifu kulinda haki zake za matangazo, akisisitiza kuwa hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi ya yeyote atakayekiuka makubaliano ya haki miliki.

Naye Mkuu wa Dawati la Michezo TBC, Evance Muhando, amesema TBC inaendelea kuwa nyumbani kwa wachambuzi na watangazaji wengi wa soka nchini, na amewakaribisha Watanzania kufurahia mashindano hayo mubashara kupitia chombo hicho cha umma.




Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) inatarajia kuandika historia mpya Julai 1, 2026 kwa kuadhimisha miaka 30 tangu kuanzishwa kwake, huku Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan, akitarajiwa kutoa Tuzo Maalum za Rais kwa Walipakodi Bora kwa mwaka wa fedha 2024/2025.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma Juni 9, 2026 kwa niaba ya Kamishna Mkuu wa TRA, Mkurugenzi wa Elimu kwa Mlipakodi na Mawasiliano, Richard Kayombo, amesema maadhimisho hayo yatafanyika chini ya kaulimbiu isemayo; “Miongo Mitatu ya TRA, Mlipakodi Shujaa, Tanzania Inayojitegemea.”

Kayombo ameeleza kuwa maadhimisho hayo yataambatana na shughuli mbalimbali za kitaifa na kikanda zitakazoanza kabla ya kilele chake Julai 1, 2026, kwa lengo la kuendelea kuimarisha ukusanyaji wa mapato ya Serikali, kuboresha huduma kwa walipakodi na kuhamasisha ulipaji kodi kwa hiari.

Amefafanua kuwa shughuli hizo zitahusisha vipindi maalum vya elimu ya kodi kupitia redio, televisheni na majukwaa ya kidijitali, kliniki za kodi, huduma za ushauri kwa walipakodi, mikutano na wadau mbalimbali wakiwemo wafanyabiashara, wahasibu na washauri wa kodi pamoja na ziara za kuwafikia walipakodi katika maeneo mbalimbali nchini.

Aidha, maadhimisho hayo yataenda sambamba na utoaji wa Tuzo ya Rais kwa Walipakodi Bora, hatua inayolenga kutambua na kuthamini mchango wa walipakodi walioonyesha uadilifu, uwajibikaji na uzalendo katika kulipa kodi na kuchangia maendeleo ya taifa.

Kwa mujibu wa Kayombo, tuzo hizo zinalenga kuimarisha utamaduni wa ulipaji kodi na kutuma ujumbe kwamba kulipa kodi si wajibu wa kisheria pekee, bali ni kitendo cha uzalendo na ushiriki wa moja kwa moja katika kujenga Tanzania yenye uchumi imara, huduma bora za kijamii na fursa zaidi kwa wananchi.

Ikumbukwe TRA ilianzishwa kwa Sheria ya Bunge mwaka 1995 na kuanza rasmi shughuli zake Julai 1, 1996, ikiwa na jukumu la kusimamia ukusanyaji wa kodi na mapato mengine ya Serikali Kuu, kuwezesha ulipaji kodi kwa hiari na kuchangia maendeleo endelevu ya kijamii na kiuchumi nchini.

Maadhimisho ya miaka 30 ya TRA yanatarajiwa kuwa jukwaa muhimu la kutathmini mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha miongo mitatu na kuweka mikakati mipya ya kuimarisha mchango wa kodi katika maendeleo ya Tanzania.






Mke wa Rais wa Singapore, Mheshimiwa Mama Jane Ittogi Shanmugaratnam, ametembelea kituo cha uzalishaji nguo za pamba zinazotengenezwa kwa mikono Msasani jijini Dar es Salaam na kujionea shughuli mbalimbali zinazofanyika katika eneo hilo.

Akiwa katika kituo hicho, Mheshimiwa Mama Jane Ittogi Shanmugaratnam alitembelea maeneo tofauti ya uzalishaji na kushuhudia hatua mbalimbali za uchakataji wa pamba hadi kutengeneza nguo zinazozingatia ubora wa hali ya juu na utunzaji wa mazingira.

Akiwa katika kituo hicho, alielezwa namna wafanyakazi wa kiwanda hicho wanavyotumia ujuzi wa jadi pamoja na teknolojia za kisasa kuzalisha bidhaa za pamba zinazokidhi mahitaji ya masoko ya ndani na kimataifa.

Mhe. Mama Jane alionesha kufurahishwa na ubunifu, ustadi na juhudi zinazofanywa na watumishi wa kiwanda hicho kidogo na wanavyotumia malighafi za ndani na kusisitiza umuhimu wa kuendeleza ushirikiano wa kimataifa unaolenga kukuza biashara, uwekezaji na maendeleo endelevu.

Rais wa Singapore, Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam na mwenza wake wako nchini kwa ziara ya siku tatu ya kitaifa ikilenga kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi, biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na Singapore.








Na Karama Kenyunko Michuzi Tv

RAIS Samia Suluhu Hassan amesema Tanzania ina fursa kubwa za uwekezaji na iko tayari kuwa lango la Singapore kuingia katika masoko ya Afrika Mashariki, Ukanda wa Maziwa Makuu na Bara la Afrika kupitia Soko Huru la Afrika (AfCFTA).

Akizungumza katika Jukwaa la Biashara na Uwekezaji la Tanzania na Singapore, Rais Samia alisema Tanzania ni moja ya nchi zenye uchumi imara na unaokua kwa kasi barani Afrika, huku ikiwa na nafasi ya kimkakati inayounganisha masoko ya Afrika Mashariki, Kati na Kusini mwa Afrika.

Alisema licha ya mahusiano mazuri ya kidiplomasia kati ya Tanzania na Singapore, bado kuna fursa kubwa ambazo hazijatumika kikamilifu katika biashara na uwekezaji.

Kwa mujibu wa Rais Samia, biashara kati ya nchi hizo iliongezeka kutoka dola za Marekani milioni 74 mwaka 2020 hadi dola milioni 299 mwaka 2023 kabla ya kushuka tena hadi dola milioni 74 mwaka 2024.

Alisema tangu mwaka 1997, Singapore imesajili miradi 36 nchini Tanzania yenye thamani ya dola milioni 535 na iliyozalisha ajira 3,328.

Rais Samia alitaja maeneo yenye fursa kubwa za ushirikiano kuwa ni bandari na usafirishaji, kilimo na usindikaji wa mazao, nishati jadidifu, miundombinu janja, utalii, uchumi wa buluu, huduma za kifedha na utatuzi wa migogoro ya kibiashara.

Alisema Tanzania ni lango la biashara kwa nchi sita zisizo na bandari ambazo ni Burundi, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Malawi, Rwanda, Uganda na Zambia, huku Bandari ya Dar es Salaam ikihudumia sehemu kubwa ya biashara hiyo.

Kwa upande wake, Rais wa Singapore, Tharman Shanmugaratnam, alisema Tanzania ni nchi yenye idadi kubwa ya vijana, rasilimali nyingi za asili, fursa zinazoongezeka za uwekezaji na nafasi ya kimkakati inayounganisha masoko ya kikanda na ya kimataifa.

Alisema ushirikiano kati ya Tanzania na Singapore unaweza kuunganisha uzoefu wa Singapore katika usimamizi wa mifumo yenye ufanisi, huduma za thamani ya juu, uchumi wa kidijitali na usimamizi wa minyororo ya ugavi na hivyo kuzalisha ajira, kuongeza ujuzi na kukuza ukuaji jumuishi wa uchumi.

Rais Samia aliwataka wafanyabiashara na taasisi za pande zote mbili kutumia jukwaa hilo kujenga ushirikiano wa kudumu utakaozalisha uwekezaji, biashara na miradi yenye manufaa kwa wananchi wa nchi hizo mbili.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Singapore, Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam mara baada ya kuwasili Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa Ziara ya Kitaifa, tarehe 09 Juni, 2026.
Na Karama Kenyunko Michuzi Tv

TANZANIA na Singapore zimefungua ukurasa mpya wa ushirikiano baada ya kusaini mikataba mitano na hati za makubaliano katika sekta mbalimbali hatua inayolenga kuimarisha biashara, uwekezaji na ushirikiano wa kiuchumi kati ya nchi hizo mbili.

Mikataba iliyosainiwa inahusi kuondoa kodi Mara mbili (Double Taxation) muendelezaji wa ujuzi, biashara za kaboni, mashauriano ya kidiplomasia na uwezeshaji wa biashara.

Mikataba hiyo itapunguza gharama za kufanya biashara, kupunguza vihatarishi vinavyotazamwa na wawekezaji na kuongeza imani kwa wawekezaji wanaotaka kuwekeza katika nchi hizo mbili.

Amesema nchi hizo pia zinaendelea kufanya kazi kuelekea mfumo wa pamoja wa utekelezaji wa biashara ya kaboni chini ya Kifungu cha sita cha Mkataba wa Paris huku zikihamasisha maendeleo endelevu.

Akizungumza katika Jukwaa la Biashara na Uwekezaji la Tanzania na Singapore jijini Dar es Salaam, Rais Tharman amesema dunia inakabiliwa na mazingira mapya ya biashara yenye kutokuwa na uhakika, hivyo kuna umuhimu wa kujenga njia mpya za ushirikiano wa kiuchumi na minyororo imara ya ugavi.

Kwa upande wake, Rais Samia Suluhu Hassan amesema yeye na Rais Tharman walifanya mazungumzo yaliyowezesha kusainiwa kwa makubaliano na hati za ushirikiano kwa manufaa ya nchi hizo mbili.

Amesema hatua hiyo inaonyesha dhamira ya pande zote mbili kuharakisha utekelezaji wa makubaliano yaliyofikiwa na kuinua uhusiano wa Tanzania na Singapore katika viwango vya juu zaidi.

Rais Samia amesema ziara hiyo ya Rais wa Singapore imekuja wakati nchi hizo zikiadhimisha miaka 45 ya uhusiano wa kidiplomasia na kwamba ni mara ya kwanza katika historia Rais wa Singapore kufanya ziara ya kiserikali nchini Tanzania.

Amesema Tanzania na Singapore zinaendelea kufurahia uhusiano mzuri unaojengwa katika misingi ya kuaminiana, ushirikiano na manufaa ya pamoja.

Na hii ni habari ya pili kuhusu fursa za biashara na uwekezaji.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiongoza Ujumbe wa Tanzania kwenye mazungumzo na Ujumbe wa Singapore uliongozwa na Rais wa Nchi hiyo Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam, tarehe 09 Juni, 2026.

Viongozi hao wawili wamefanya mazungumzo rasmi yaliolenga kuimarisha ushirikiano kati ya Tanzania na Singapore katika maeneo mbalimbali hususani biashara, uwekezaji, maendeleo ya rasilimali watu na ujuzi, pamoja na uchumi wa kidijitali.Mazungumzo hayo yalifuatiwa na utiaji saini wa mikataba na Hati za ushirikiano kati ya nchi hizo mbili, na mkutano wa pamoja na waandishi wa habari.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Singapore, Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam kwenye mkutano na Waandishi wa Habari uliofanyika, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 09 Juni, 2026.



Mstahiki Meya wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Alimwoni Chaula, amefanya ziara ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa Barabara ya Kidia, ambayo ni miongoni mwa barabara zinazoboreshwa kwa kiwango cha lami katikati ya Jiji la Dodoma.

Ujenzi wa barabara hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mh. Dk. Samia Suluhu Hassan, ya kutaka halmashauri za majiji kutenga asilimia 10 ya mapato ya ndani kwa ajili ya ujenzi na uboreshaji wa barabara za mitaa.

Akizungumza wakati wa ukaguzi huo, Mstahiki Meya Chaula aliwataka wananchi kushiriki katika kutunza miundombinu hiyo ili iweze kudumu na kuendelea kutoa huduma kwa muda mrefu.

“Wananchi kwa pamoja tunapaswa kushirikiana katika kuzitunza barabara hizi kwa kufuata taratibu zilizowekwa,Wafanyabiashara waepuke kufanya biashara katika maeneo ya barabarani kwani hali hiyo huchangia uharibifu wa miundombinu hiyo” alisema Chaula.

Aliongeza kuwa halmashauri itaendelea kutoa elimu kwa wafanyabiashara kupitia viongozi mbalimbali wa maeneo husika kuhusu athari za kufanya shughuli za biashara kwenye hifadhi ya barabara.

Kwa upande wake, mfanyabiashara wa eneo hilo, Peter Moshi ameishukuru serikali kwa kutekeleza mradi huo akisema kuwa wananchi walikuwa wakisubiri kwa muda mrefu kuona barabara hiyo ikiboreshwa na kukamilika kwake kutarahisisha shughuli za biashara, kuongeza usafiri wa uhakika na kuchochea maendeleo ya kiuchumi kwa wakazi wa eneo hilo na maeneo jirani.

Barabara zinazotekelezwa katika mpango huo zina jumla ya urefu wa kilometa moja kila moja na zinagharimu takribani shilingi bilioni 1.9 kwa ujumla.







Na Janeth Raphael MichuziTv 


Tanzania na Singapore zimekubaliana kuimarisha na kupanua ushirikiano wao katika nyanja za uchumi, biashara na uwekezaji, katika hatua inayolenga kuongeza tija na manufaa kwa wananchi wa mataifa hayo mawili.

Makubaliano hayo yamefikiwa kufuatia mazungumzo rasmi kati ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, na Rais wa Jamhuri ya Singapore, Tharman Shanmugaratnam, ambaye yupo nchini kwa ziara ya kitaifa ya kihistoria.

Akizungumza leo Jumanne, Juni 09, 2026, baada ya kumpokea mgeni huyo Ikulu, Rais Samia amesema mazungumzo yao yamejikita katika namna bora ya kuimarisha ushirikiano uliopo ili ulete matokeo halisi katika maendeleo ya pande zote mbili.

Amebainisha kuwa licha ya kuwepo kwa ukuaji wa mahusiano ya kibiashara, bado kiwango cha biashara kati ya Tanzania na Singapore hakijafikia matarajio ya nchi hizo. Kwa sasa, biashara kati ya mataifa hayo inakadiriwa kufikia takribani dola za Marekani milioni 299, huku Singapore ikiwa tayari imewekeza kupitia miradi 36 nchini Tanzania.

Rais Samia amesema makubaliano mapya yanalenga kuongeza mtiririko wa biashara, kuvutia uwekezaji zaidi, na kufungua fursa mpya katika sekta mbalimbali muhimu za kiuchumi.

Katika upande wa diplomasia, Tanzania imeiomba Singapore kufungua ubalozi wake nchini, hatua inayotarajiwa kuimarisha zaidi mahusiano ya kidiplomasia na kiuchumi kati ya nchi hizo.

Aidha, viongozi hao wamekubaliana kuanzisha mfumo wa mashauriano ya mara kwa mara utakaosaidia kuratibu mipango ya maendeleo na kushughulikia changamoto zinazoweza kujitokeza katika utekelezaji wa miradi ya ushirikiano.

Katika sekta ya kilimo, Tanzania imeonesha dhamira ya kushirikiana na Singapore katika kuimarisha usalama wa chakula, hatua itakayosaidia kuongeza biashara ya mazao ya chakula pamoja na kuhakikisha upatikanaji wa chakula cha kutosha na cha uhakika kwa pande zote mbili.

Rais Samia pia amesisitiza umuhimu wa kuwawezesha vijana, akibainisha kuwa Dira ya Taifa 2050 imeweka msingi mkubwa wa kuwajenga vijana kama nguzo ya maendeleo ya taifa katika miaka ijayo.

Ziara ya Rais Tharman Shanmugaratnam imeelezwa kuandika ukurasa mpya katika historia ya mahusiano ya Tanzania na Singapore, ikiwa ni mara ya kwanza kwa Rais wa Singapore kufanya ziara ya kitaifa nchini Tanzania tangu kuanzishwa kwa uhusiano wa kidiplomasia kati ya mataifa hayo mawili.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Rais wa Jamhuri ya Singapore, Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam mara baada ya kuwasili Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa Ziara ya Kitaifa, tarehe 09 Juni, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiongoza Ujumbe wa Tanzania kwenye mazungumzo na Ujumbe wa Singapore uliongozwa na Rais wa Nchi hiyo Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam, tarehe 09 Juni, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Waandishi wa Habari kuhusu Ziara ya Kikazi ya Rais wa Jamhuri ya Singapore, Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 09 Juni, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Singapore, Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam akizungumza na Waandishi wa Habari kufuatia Ziara yake ya Kitaifa Jijini Dar es Salaam, tarehe 09 Juni, 2026.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na Rais wa Jamhuri ya Singapore, Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam mara baada ya kuwasili Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa Ziara ya Kitaifa, tarehe 09 Juni, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Singapore, Mheshimiwa Tharman Shanmugaratnam, ambaye amewasili nchini kwa ziara ya Kitaifa ya siku 3, kufuatia mwaliko wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na mwenyeji wake mara baada ya kuwasili ikulu.

Mheshimiwa Rais Tharman Shanmugaratnam ameweka historia ya kuwa Rais wa kwanza kutembelea nchini tangu kuanzishwa kwa mahusiano ya kidiplomasia mwaka 1980.








Top News