Na Mwandishi Wetu

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe Albert Chalamila leo Feb 23,2026 akiwa ameambatana na kamati ya usalama Mkoa, amesaini kitabu cha maombolezo kufuatia kifo cha Askofu Mkuu mstaafu wa Jimbo la Dar es Salaam Mwadhama Cardinali Polycarp Pengo Kurasini Jijini humo.

Aidha Mkuu wa Mkoa pamoja na Kamati ya usalama alieleza masikitiko yake makubwa na kutoa rambirambi, kwa familia, Kanisa Katoliki na Taifa kwa ujumla ambapo amesema anamuomba mwenyezi Mungu aipumzishe roho ya marehemu mahala pema peponi Amina.

Ifahamike kuwa maziko ya Mwadhama Cardinali Polycarp Pengo yanatarajiwa kufanyika Feb 28, 2026 Pugu Jijini Dar es Salaam kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kanisa Katoliki Jimbo Kuu la Dar es Salaam.



*📌 Bilioni 6.8 zaongeza matumaini ya nishati safi Kisemvule, Pwani*

*📌 Wananchi wengi zaidi kusambaziwa gesi asilia kwa mkoa wa Pwani na Lindi*

Kisemvule, Pwani📍

Utekelezaji wa mradi wa kusambaza gesi asili katika eneo la Kisemvule, wilayani Mkuranga mkoani Pwani, umeendelea kuibua matumaini mapya kwa Wananchi wa eneo hilo ambapo zaidi ya shilingi bilioni 6.8 zimewekezwa katika kusambaza gesi asilia katika maeneo yaliyopitiwa na mkuza wa bomba la gesi asilia.

Mradi huo umejengwa na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) na kufadhiliwa na Wakala wa Nishati Vijijini (REA) umeelezwa kuwa ni sehemu ya mkakati wa Serikali ya Awamu ya Sita wa kuhakikisha ifikapo mwaka 2034 asilimia 80 ya Watanzania watakuwa wanatumia nishati safi ya kupikia.

Akizungumza baada ya kutembelea na kukagua Mradi huo; Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB), Mhe. Balozi na Meja Jenerali Mstaafu, Jacob Kingu, amesema utekelezaji wa Mradi huo unaonesha dhamira ya dhati ya Serikali katika kuboresha maisha ya Wananchi na kulinda mazingira.

Amesema Bodi ya Nishati Vijijini inajivunia kuona mwitikio mkubwa wa Wananchi wanaene kuhamasika kuachana na matumizi ya kuni na mkaa na badala yake kutumia gesi asili, ambayo ni salama, nafuu na rafiki kwa mazingira.

“Huu ni Mradi wa kimkakati unaotekeleza maono ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuona Watanzania wengi wanatumia nishati safi, tunapaswa kulinda miundombinu hii kwa kuwa imegharimu fedha nyingi za Serikali,” amesema Balozi Kingu.

Kwa mujibu wa REA, mradi huo wa mfano ulilenga kuhudumia kaya 2,000 huku hadi sasa kaya 530 zikiwa zimefikiwa na huduma hiyo katika eneo la Kisemvule lenye wakazi zaidi ya 64,000 hali inayotoa fursa ya kupanua zaidi wigo wa huduma hiyo.

Mkurugenzi Mkuu wa REA, Mhandisi, Hassan Saidy amesema taasisi hiyo imeiomba TPDC kufanya tathmini katika maeneo yenye idadi kubwa ya watu ambako bomba la gesi limepita ili kuanzisha miradi ya ubia itakayowezesha wananchi wengi zaidi kuunganishwa na huduma hiyo.

Ametaja baadhi ya maeneo yanayopendekezwa kuwa ni Mkuranga Mjini, Ikwiriri na Kilwa Kivinje, akibainisha kuwa hatua hiyo itaharakisha utekelezaji wa Sera ya Nishati Safi nchini.

Naye Mkurugenzi wa Nishati Jadidifu na Teknolojia za Nishati Mbadala kutoka REA, Mhandisi, Advera Mwijage amesema Bodi ya Nishati Vijijini imeagiza kuongeza kasi ya uunganishwaji wa kaya zaidi ili Mradi huo unufaishe Wananchi wengi zaidi kulingana na mahitaji halisi ya eneo hilo.

Kwa upande wake, Mhandisi, Tumaini Daniel, Meneja Mradi kutoka TPDC amesema Mradi huo umekamilika kwa mafanikio na umeweka msingi mzuri wa upanuzi wa huduma hiyo katika maeneo mengine yenye miundombinu ya bomba la gesi.

Wananchi wa Kisemvule wameanza kunufaika matokeo chanya ya Mradi huo, wakieleza kupungua kwa gharama za matumizi ya nishati na urahisi wa upatikanaji wa gesi asilia kupitia mifumo ya malipo ya simu.

Mradi huo unaendelea kuwa mfano wa utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Nishati Safi ukionesha namna uwekezaji wa kimkakati unavyoweza kubadilisha maisha ya Wanancha ili kulinda mazingira na kuchochea maendeleo ya kiuchumi katika ngazi ya jamii.






 

Mamlaka ya Udhibiti wa Nafaka na Mazao Mchanganyiko (COPRA) imeendesha mafunzo maalum kwa Maafisa Ugani 128 wa Mkoa wa Arusha kwa lengo la kuimarisha uzalishaji endelevu na ubora wa mazao ya kimkakati.

Mafunzo hayo yamefanyika kwa ushirikiano kati ya wataalamu wa COPRA, KILICCERT pamoja na Ofisi ya Mkoa wa Arusha, yakilenga kuwajengea uwezo maafisa ugani katika kusimamia na kushauri wakulima kwa ufanisi zaidi.

Kupitia mafunzo hayo, washiriki wamepata maarifa kuhusu: ✅ Viwango vya Uzalishaji Endelevu

✅ Kilimo bora cha mazao ya ufuta na mikunde

✅ Matumizi ya miongozo ya kilimo endelevu iliyoandaliwa na COPRA

✅ Uzingatiaji wa ubora wa mazao kulingana na mahitaji ya soko

Lengo kuu la COPRA ni kuhakikisha mazao yanayozalishwa yanakidhi viwango vya kitaifa na kimataifa, hivyo kuongeza ushindani wa wakulima katika masoko ya ndani na nje ya nchi.

Hatua hii inaonesha dhamira ya COPRA katika kuinua sekta ya kilimo kwa kuimarisha maarifa ya maafisa ugani ambao ni kiungo muhimu kati ya wataalamu na wakulima mashinani.








Na mwandishi wetu, Tanga.
Watumishi wa Wizara ya Nishati wameipongeza Serikali na Wanahisa wengine wa EACOP kwa kutoa fedha za kutekeleza mradi mkubwa wa kimkakati wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP). Pamoja na pongezi hizo Kampuni ya EACOP imepongezwa kwa kuzingatia uhifadhi wa mazingira katika hatua zote za utekelezaji wa mradi hususani viumbe hai katika maeneo yote yanayopitiwa.

Kauli hiyo imetolewa Februari 22, 2026, Chongoleani, Tanga na mwakilishi wa watumishi hao Bw. Benson Lukuta akiwa Mkuu wa Msafara katika ziara iliyofanywa na watumishi wa Wizara ya Nishati kutembelea mradi huo.

Bw. Lukuta pia kwa niaba ya watumishi aliushukuru Uongozi wa Wizara kwa kufanikisha ziara hii muhimu kwa watumishi kufahamu na kujione Miradi inayosimamiwa na Wizara.

Ziara hiyo ililenga kujionea maendeleo ya utekelezaji wa mradi huo mkubwa, hususan jinsi unavyozingatia uhifadhi wa mazingira, ulinzi wa viumbe hai katika maeneo yanayopitiwa na manufaa kwa jamii katika maisha ya kila siku na ujuzi.

“Utekelezaji wa mradi huu wa kimkakati umezingatia sana uhifadhi wa mazingira na kuleta manufaa kwa jamii zinazouzunguka. Mradi huu unaounganisha Tanzania na Uganda na ni mojawapo ya miradi mikubwa katika ukanda wa Afrika Mashariki, ukiwa na lengo la kusafirisha mafuta ghafi kutoka Hoima, Uganda hadi Bandari ya Tanga, Tanzania,” alisema Lukuta.

Kwa upande wake, Bw. Thomas De Mauleon Mwakilishi wa Kampuni ya EACOP, alisema mradi huo una manufaa makubwa kwa Watanzania, si tu kiuchumi bali pia kijamii na kitaalamu.

Aidha, amesema mpaka sasa mradi umeweza kutoa ajira za moja kwa moja kwa Watanzania 10,000, huku wananchi 170 wakipatiwa mafunzo maalum ili kufikia viwango vya kimataifa katika ujenzi wa miradi ya mafuta na gesi.

Pia, kupitia miradi ya kijamii, EACOP imeboresha barabara na huduma za maji katika maeneo yanayopakana na Mradi. Takribani kilomita 27 za barabara za changarawe zimeboreshwa, zikiwemo: Barabara ya Kagongwa hadi Sojo (km 18), Handeni kuelekea Kambi Na. 15 (km 2.1), barabara ya kuunganisha eneo kuu la Mradi Chongoleani (km 7.2).

Hatua hizi zinaongeza urahisi wa usafirishaji, kuunganisha jamii na kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi katika maeneo yanayopitiwa na mradi.








Na Mwandishi Wetu

Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) kimeanza  kukutana na jumuiya za shule na Wanafunzi Jiji la Dodoma kwa lengo la kuhamasisha ufaulu hasa katika masomo ya Sayansi.

 Mhadhiri Msaidizi wa Chuo hicho na Mwalimu wa Hesabu  Dorothy Manoza amesema kuwa jamii imechukulia kama somo la hesabu limekuwa ni shida katika uelewa na kusahau kuwa somo hilo ni somo kama masomo mengi.

 Dorothy ameyasema hayo leo Jijini Dodoma Februari 23,2026 katika Shule ya Sekondari Chinangali ambapo Wataalam kutoka NIT wapo katika ziara ya kutembelea baadhi ya shule za Sekondari ikiwemo Drt Samia,Bunge,Hazina,Bihawana,Chinangali na Wella za Jiji la Dodoma ili kuongea na wanafunzi na jumuiya za shule kuhamasisha kuongeza ufaulu katika masomo yao hasa masomo ya Sayansi na kjiunga na fani za masomo hayo wanapojiunga na masomo ya Elimu ya juu.

Ameongeza kuwa wakati mwingine watoto kuogopa Hesabu ni kutokana na   kukosa msingi mzuri wa somo hilo,lakini pia wazazi kutowatia moyo watoto hasa mabinti kwasababu tofauti tofauti bila kujua kwamba dunia ya sasa ni ya Sayansi na Teknolojia na hakuna Teknolojia pasipo Hisabati.

"Kweli jamii imekuwa na changamoto ya kuliona kama somo la hesabu ni shida katika uelewa lakini ni kitu ambacho sio sahihi hesabu ni somo kama masomo mengine na unaweza ukafanikiwa kama unavyofanikiwa katika masomo mengine".

Naye Afisa Uhusiano Chuo cha Taifa cha Usafirishaji Juma Mandai ameeleza kuwa wamekuja kuhamasisha umuhimu wa masomo ya Sayansi kwasababu chuo hicho kinatoa kozi inayoenda na miradi mikubwa na ya kimkakati inayotekelezwa na Serikali na kuhitaji rasilimali watu na Wataalam hususan wazawa ambapo katika miradi hiyo kumekuwa na upungufu wa Wataalamu hasa wazawa wanaoweza kusimamia miradi hiyo.

Na kusema kuwa hicho ndicho kilichowapelekea kuona umuhimu wa wao kama chuo chenye dhamana ya kuzalisha rasilimali watu katika sekta ya Usafirishaji na Uchukuzi kupita katika shule za Sekondari kuhamasisha wanafunzi wapende masomo ya Sayansi na wajue fursa zilizopo katika masomo hayo na kozi zitakazo wasaidia kupata ajira katika sekta hiyo ya Usafirishaji na Uchukuzi.

"Chuo chetu ni cha kisekta kiko chini ya  Wizara ya Uchukuzi,tunatoa kozi ambayo inaendana na miradi mikubwa ambayo Serikali inatekeleza kwasasa,miradi ya kimkakati na miradi hii inahitaji nguvu ya rasilimali watu na wataalam ambapo hao wataalam sasa hususan ni wazawa ambapo katika baadhi ya miradi kuna upungufu wa wataalam wazawa ambao wanaweza kusimamia hii miradi ya kimkakati ya Serikali yetu inayotekeleza sasa".

Kwa upande wake Mkuu wa Shule ya Sekondari Chinangali Victor Salisali mbali na kuwashukuru NIT kama wadau wao wa muda mrefu ambao wamekuwa wakiwapatia walimu wa somo la hesabu amesema kuwa ukiangalia masomo ya sayansi yamekuwa na walimu na wanafunzi wachache ila kwa ujio wa NIT utakwenda kuongeza hamasa ya kuwa wanafunzi wengi katika masomo ya Sayansi. 

Pamoja na kutoa wito kwa wanafunzi wote kutambua kuwa dunia ipo katika Teknolojia kutoka analogy kwenda digitali hivyo wanatakiwa kuhamasika kufanya au kusoma masomo ya sayansi zaidi ili kuendana na mabadiliko ya Sayansi na Teknolojia. 

"Kwa kawaida ukiangalia Walimu wa masomo ya sayansi ni wachache na wanafunzi wanaosoma masomo ya sayansi ni wachache pia, kwahiyo kwa kufika kwenu NIT na kuongea nao nafikiri itakuwa ni hamasa kwao lakini pia tunategemea tutakuwa na wanafunzi wengi ambao watasoma masomo ya Sayansi".

Salim Hassan ambaye ni Kaka Mkuu wa Sekondari hiyo amesema kuwa ujio wa ugeni wa NIT umekuja kuongeza chachu katika masomo ya Sayansi kwa kuwasaidia wale wanaodhani kuwa masomo ya Art tu ndo mapesi hivyo watapendelea masomo ya Sayansi kwani ndio yenye fursa ya ajira.

Naye Sakina Mustapha ambye ni Dada Mkuu katika Shule hiyo pia amesema kuwa hamasa hiyo ya leo inaweza kuhamasisha wanafunzi wengi wakachukua mchepuo wa Sayansi kwasababu NIT imeelezea jinsi mchepuo wa Sayansi ulivyorahisi na utakavyoweza kuja kufanikiwa kuwa Injinia,Rubani na hata kuwa Muhudumu wa Usafiri wa Anga.

Wataalam wa Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) watakuwa na ziara ya siku 5 kuanzia leo tarehe 23 hadi tarehe 27 februari 2026 na kutembelea Shule 11 za Sekondari kwa Jiji la Dodoma.







Vikwazo vitano visivyo vya kikodi kati ya kumi vilivyokuwa vikisababisha msongamano mkubwa wa malori na usumbufu kwa wafanyabiashara na wasafirishaji katika mpaka wa Tunduma/Nakonde, zimepatiwa ufumbuzi kupitia juhudi za pamoja za Serikali za Tanzania na Zambia. Hatua hiyo inatajwa kuwa chachu ya kuimarisha biashara za kimataifa katika ukanda wa Kusini mwa Afrika.

Maamuzi hayo yamefikiwa katika kikao cha ujirani mwema kilichofanyika mpakani Tunduma na kuwakutanisha Mawaziri wa Mambo ya Nje kutoka pande zote mbili, wakiongozwa na Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb.) kwa upande wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mhe. Mulambo Haimbe(Mb.)kwa upande wa Zambia.

Akizungumza na waandishi wa habari baada ya kikao hicho, Waziri Kombo ameeleza kuwa moja ya mafanikio makubwa ni kuridhia kwa serikali ya Zambia kuanza kutoa huduma kwa saa 24 kama ilivyo katika utaratibu wa Kituo cha Pamoja - One Stop Border Post (OSBP), hatua hii itakayopunguza kwa kiasi kikubwa ucheleweshaji wa mizigo na msongamano wa magari ya mizigo katika eneo hilo.

Aidha, Zambia imekubali kutumia mashine ya kisasa ya mdaki (scanner) iliyotolewa na Serikali ya Tanzania ili kuongeza kasi na ufanisi katika ukaguzi wa mizigo, jambo litakalorahisisha uvukaji wa malori na kupunguza gharama za ucheleweshaji kwa wafanyabiashara.

Katika kuimarisha ushirikiano wa kiteknolojia, pande hizo mbili pia zimekubaliana kusomanisha mifumo ya forodha ya TANCIS inayotumika Tanzania na ASYCUDA Plus inayotumika Zambia, ili kuwezesha ubadilishanaji wa taarifa kwa haraka na kuongeza uwazi katika shughuli za mpakani.

Hatua hizi zinatarajiwa kuongeza ushindani wa bandari na mipaka ya Tanzania, kuchochea biashara za kikanda na kimataifa, na kuimarisha uchumi wa nchi zote mbili pamoja na ukanda wa Kusini mwa Afrika kwa ujumla.



















Na FARIDA MANGUBE MOROGORO

Waziri wa Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji, Kitila Mkumbo, ameweka wazi kuwa kilimo kinabaki kuwa sekta muhimu ya uchumi wa taifa na kwamba ili kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, ni lazima sekta hiyo ilindwe, itunzwe na kuendelezwe kwa ushirikiano wa dhati kati ya wananchi, serikali, na wawekezaji.

Waziri Mkumbo ametoa kauli hiyo wakati wa ziara yake ya kikazi Mkoani Morogoro ambapo amekagua maendeleo ya uwekezaji wa kilimo katika maeneo hayo.

Katika ziara hiyo, Waziri Mkumbo alijikita zaidi katika kuimarisha ulinzi wa miundombinu ya kilimo, akisema kuwa serikali inatoa kipaumbele kwa kilimo cha kibiashara, ambacho kimejikita katika uzalishaji wa mazao ya mtama, mahindi, miwa, ufuta na alizeti.

Amesisitiza kuwa, licha ya kuwa na ardhi kubwa inayofaa kwa kilimo, bado Tanzania inakosa tija, huku sehemu kubwa ya ardhi hiyo ikiwa haijalimiwa.

“Tunahitaji ushirikiano wa kila mmoja. Bila usalama, kilimo cha kibiashara hakiwezi kustawi. Wawekezaji hawa wamewekeza fedha nyingi, lakini changamoto hizi zinapunguza tija na athari zake ni kubwa kwa uchumi wetu,” alisema Mkumbo.

Aliongeza kuwa, kwa upande wa serikali, miongozo ya kisera imejikita katika kuboresha mazingira ya biashara, lakini bila ushirikiano wa jamii na wawekezaji, juhudi hizo zitakuwa bure. Alisema kuwa, kilimo kimekuwa sekta ya kujikimu kwa muda mrefu, lakini sasa serikali inalenga kuhamasisha kilimo cha kibiashara, ili kuongeza uzalishaji wa mazao na kutoa ajira kwa wananchi wengi.

Madiwani wa kata za Matuli na Mkulazi wamekiri changamoto zinazozikumba sekta ya kilimo, lakini walisisitiza kuwa jamii ina nafasi kubwa katika kuhakikisha kuwa changamoto hizi zinatatuliwa.

Madiwani hao walieleza kuwa, ili kufanikisha mabadiliko ya kilimo cha kibiashara, ni lazima wananchi washirikiane kwa karibu na wawekezaji na mamlaka za serikali.

“Kilimo ni fursa kubwa kwa wananchi wetu. Lakini ili kufanikisha hili, tunahitaji kushirikiana na wawekezaji ili kuimarisha usalama wa maeneo ya uzalishaji na kuhakikisha kilimo kinakuwa na tija,” alisema Lucas Lemono, Diwani wa Kata ya Matuli.

Katika kuimarisha kilimo cha kibiashara, Waziri Mkumbo amesema kuwa Serikali itaendelea kutekeleza mkakati wa kuvutia wawekezaji wa ndani na nje, kwa kutoa mikopo nafuu na mafunzo kwa wakulima wadogo, huku ikiwataka wawekezaji kutumia teknolojia za kisasa ili kuongeza uzalishaji na tija.

Amesisitiza kuwa ili kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, sekta ya kilimo inahitaji uwekezaji wa kutosha katika mashamba makubwa, matumizi ya teknolojia za kisasa, na mitaji ya kutosha.

“Kilimo cha kisasa kinahitaji vifaa vya kisasa, mbegu bora, na mifumo ya umwagiliaji.

Wawekezaji hawa wanatakiwa kusaidia wakulima wadogo kwa kuwapa mafunzo na mitaji, na serikali iko tayari kutoa msaada wote unaohitajika,” alisema Mkumbo.

Meneja Mkuu wa Santagro Ltd, Luab Luiz de Carvalho, ameiomba serikali Kumalizia changamoto ya muingiliano kati yao na wafugaji ambapo wafugaji wamekuwa wakiingiza Mifugo shambani na kulisha mazao. Alisema kuwa, licha ya kuwa na miundombinu imara, mifugo ni tishio kubwa kwa uwekezaji wao.

“Tunahitaji msaada wa haraka kutoka kwa serikali na jamii kuhakikisha mifugo inadhibitiwa. Bila ulinzi wa kutosha, hakuna uwekezaji wa maana utakaofaidi jamii,” alieleza de Carvalho.

Ziara hiyo pia ilihudhuriwa na Mkuu wa Wilaya ya Morogoro, Mussa Kilakala, ambaye alihakikishia wawekezaji kuwa, pamoja na changamoto, Wilaya ya Morogoro ni eneo salama la uwekezaji na kwamba usalama wa maeneo ya kilimo utadumishwa kwa nguvu zote.




Top News