Mkuu wa mkoa wa Geita ametangaza rasmi kutokuwa na mwekezaji katika eneo la uwanja wa mpira wa CCM, eneo ambalo lilibua taharuki baina ya serikali ya Kijiji na chama Cha mapinduzi.

Ikumbukwe kuwa mnamo January 24 Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu TAMISEMI Mhe Riziki Shemdoe aliuagiza uongozi wa wilaya ya Geita Chini ya mkuu wa mkoa wa Geita kuhakikisha ndani ya siku 14 unawasilisha taarifa ya kina kuhusu mgogoro unaomhusisha mwekezaji aliyedaiwa kubomoa maeneo ya serikali na kuanzisha miradi bila utaratibu.

Akiongea na wananchi katika mamlaka ya mji mdogo wa Katoro mkuu wa mkoa wa Geita Martin Shigela amesema kuwa mwekezaji ambaye alitajwa na kuwekeza katika eneo la chama Cha mapinduzi hakuwa na Mikataba ya kuwekeza katika eneo Hilo.

Shigela amewataka wananchi kuwa watulivu na kusubiri majibu ya vikao vya ndani baina ya chama na serikali ambapo ameongeza kuwa eneo Hilo halipaswi kubadilishwa matumizi ambapo hapo awali eneo hilo lilitumika kama eneo la Michezo

Januari 23,2026 kamati ya FEDHA na uchumi ya halmashauri ya wilaya ya Geita ilifika katika eneo Hilo na kubaini kwamba mwekezaji tajwa alikuwa akiendelea na shughuli za kuanzisha mradi wake bila ya kuwa na vibali ,hali iliyoibua taharuki Kati ya mwekezaji huyo na wajumbe wa kamati hiyo iliyoongozwa na mwenye kiti wa halmashauri ya wilaya ya Geita Jumanne Misungwi.

Nae mbunge wa Jimbo la Katoro Mhandisi Kija Limbu Ntemi ameushukuru uongozi wa mkoa kwa kusimamia swala hilo ambalo lilianza kuleta taharuki kwa wananchi waishio maeneo hayo

 

Serikali yazindua Sera ya Taifa ya Kinga ya Jamii na ‘Hifadhi Scheme’ kwa Waliojiajiri

Na MWANDISHI WETU, 

ARUSHA. Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Mahusiano imezindua Sera ya Taifa ya Kinga ya Jamii pamoja na Mpango wa Hifadhi ya Jamii kwa Wananchi Waliojiajiri ‘Hifadhi Scheme’ hatua inayolenga kupanua wigo wa hifadhi ya jamii na kuongeza ushirikishwaji wa wananchi katika mifumo ya kinga ya kijamii.

Uzinduzi huo umefanyika Februari 9, 2026 katika mkutano wa wadau wa sekta ya kinga ya jamii uliofanyika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Arusha (AICC), ukiongozwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu kwa niaba ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Sangu alisema sera hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, inayolenga kuhakikisha wananchi wanapata huduma jumuishi za hifadhi ya jamii. Aliongeza kuwa tangu 2018, Serikali imefanya maboresho ikiwemo kuunganisha Mifuko ya Hifadhi ya Jamii na kubaki na NSSF na PSSSF ili kuongeza ufanisi wa huduma na ulipaji wa mafao.

Mhe. Sangu alisema maboresho hayo yameongeza idadi ya wanachama. NSSF imeongezeka kutoka wanachama 808,935 mwaka 2020 hadi zaidi ya wanachama 2,213,659 mwaka 2025, huku PSSSF ikiongezeka kutoka 697,677 hadi 899,948. Aidha, thamani ya uwekezaji wa Mifuko imeongezeka kutoka shilingi trilioni 9.36 hadi trilioni 20.14, na jumla ya thamani ya Mifuko kufikia trilioni 24.20.

Kuhusu mpango wa Hifadhi Scheme, alisema hadi Desemba 2025 zaidi ya wanachama 500,000 kutoka makundi mbalimbali yakiwemo wakulima, wafugaji, wavuvi na wajasiriamali wamejiunga, huku lengo likiwa kufikia wanachama milioni 5.5 ifikapo Juni 2031.

Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Mary Maganga, alisema Serikali imeipa NSSF jukumu la kupanua wigo wa hifadhi ya jamii kwa wananchi waliojiajiri ili kuhakikisha sera mpya inaleta matokeo yanayotarajiwa.

Awali, Mkurugenzi Mkuu wa NSSF, Bw. Masha Mshomba, alisema Mfuko unaendelea kuboresha utoaji wa huduma, kuongeza uandikishaji wa wanachama wapya, na kupanua wigo wa uwekezaji ndani na nje ya nchi, ikiwemo nchi za SADC na Afrika Mashariki.

Bw. Mshomba alisema Mfuko umepata mafanikio makubwa katika Serikali ya awamu ya sita ambapo thamani ya NSSF imeongezeka kutoka trilioni 4.8 mwaka 2021 hadi trilioni 10.4 Desemba 2025, na kuwa imepata ziada kwa miaka minne mfululizo kuanzia 2021 hadi mwaka wa fedha 2024/25, ikivuka lengo la ziada ya shilingi trilioni moja.

Akizungumzia ukusanyaji wa michango, Bw. Mshomba alisema Mfuko umeendelea kuvuka malengo, ambapo mwaka wa fedha 2023/24 ulifikia zaidi ya shilingi trilioni mbili, huku mwaka 2024/25 makusanyo yakizidi trilioni 2.4 na kwamba katika kipindi cha miaka mitano mfululizo kuanzia 2020 hadi 2025, NSSF imefanikiwa kuvuka lengo la kukusanya angalau shilingi trilioni moja kwa mwaka. 

Bw. Mshomba aliongeza kuwa mafanikio hayo yamechangiwa na juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan. NSSF ina zaidi ya wanachama milioni 2.3 na imejikita kuboresha huduma kupitia TEHAMA na mpango wa miaka mitano unaolenga kufanikisha malengo ya Dira ya Taifa 2050 na Ilani ya Uchaguzi ya CCM. 



Na. Vero Ignatus Arusha.


Mkutano wa siku mbili wa Wadau wa Kinga ya jamii umefanyika leo Februari 9,2026 Jijini Arusha ambapo umehudhuriwa na wadau zaidi ya 1000 kutoka Tanzania Bara na Visiwani ambapo umeambatana na uzinduzi wa Sera ya Taifa ya Kinga ya Jamii, katika Kituo cha Kimataifa cha AICC Mkoani hapa.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa Sera hiyo Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano), Deus Sangu amesema miongoni mwa wadau wakubwawa sekta ya ya kings ya Jamii ni walioshiriki katika mkutano huo ni pamoja na PSSSf ambapo.imeweza kuongeza idadi ya wanachama kutoka 697,677 juni 2020 Hadi kufikia 889,948 disemba 2025

Sangu, aliwataka wadau wa mifuko ya hifadhi ya jamii kuimarisha utoaji wa huduma kwa kuhakikisha taarifa za wanachama zinakuwa sahihi na waajiri wote wanawasilisha michango kwa wakati ili kuepusha usumbufu kwa wanachama.

"Mifuko iimarishe utoaji wa huduma kwa kuhakikisha taarifa za wanachama zipo sahihi na waajiri wote wanawasilisha michango kwa wakati katika hili kila mwajiri atekeleze wajibu wake ."'alisema Sangu.

Sangu amesema thamani ya mfuko PSSSf ineongezeka kutoka trillion 5.66 juni 2020 hadi kufikia trillion 10.51 seaemba 2025 na kusema kuwa Serikali ya awamu ya sita iliahidi kwamba Sera hiyo itahakikusha kuwa hakuna Mtanzania atakayebakia nyuma atakapopata changamoto kama ulemavu, umaskini uzee,majanga ya asili ukosefu wa ajira

"Hivyo basi mifuko yote ikiwemo PSSSf, NSSF na WCF imeongezeka kutoka trillion 10.43 june 2020 hadi kufikia trillion24. 20desemba 2025

Kwa upande wake mkurugenzi Mkuu Wa PSSSf ndugu Fortuatus Magambo ameseema kwamba wapo mstari Wa mbele katika kutekeleza kwa vitendo Sera ya Taifa ya kinga ya Jamii na kuendelea kuwahudumia wanachama wao, huku akisema katika kipindi cha nusu mwaka. Julai hadi disemba 2025 PSSSf iliingiza katika mzunguko Wa fedha kwa njia ya ulipaji Wa mafao sh. Bilioni 883.

Akitoa salamu za Bunge kwa niaba ya Mhe. Hawa mchafu Chakoma Mwenyekiti wa Kamati ya kudumu ya Bunge ya ustawi na maendeleo ya Jamii akimuwakilisha Spika wa Bunge la Jamhuri ya Tanzania Hassan Zungu amesema Bunge linalo jukumu la kutunga sheria mbalimbali kwa kusimamia kanuni miongozo na Sera

Mkurugenzi Mkuu wa NSSF Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), Bw. Masha Mshomba, amesema hakuna sababu kwa mwananchi aliyejiajiri kushindwa kujiunga na Mfuko huo kutokana na maboresho makubwa yaliyofanywa ambayo yanawawezesha kunufaika na mafao mbalimbali sawa na waajiriwa wa sekta ya umma na binafsi.

Mshomba amesema kuwa thamani ya mfuko NSSF imeongezeka kutoka trillion 4.36 juni 2020 hadi, zkufikia trillion 10.40 disemba 2025 ambapo awali walikuwa wanawekeza trilliin 3.14 2020 - disemba 2025 trillion 8.74

Alisema mwananchi atakayejiajiri na kujiunga na NSSF atanufaika na mafao ya pensheni ya uzeeni, urithi, ulemavu, uzazi, matibabu pamoja na mafao mengine ambayo awali hayakuwa yakipatikana kwa kundi hilo.

Ikumbukwe kuwa mwaka 2018 Serikali ilifanya maboresho katika sekta ya kinga ya Jamii NCHINI ikaweza kuunfanisha mifuko iliyokuwepo na kubakisha mifuko miwili mmoja kwaajili ya Sekta ya I'mma (PSSSF) na mfuko mwingine kwaajili ya Sekta binafsi (NSSF) ambapo mabadilliko hayo yalifanyika ili kuleta ufanisi katika uendeshaji.








Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira NEMC Leo Februari 9, 2026 limekifunga kiwanda cha urejelezaji wa taka za plastiki cha HOOTA kilichopo Kata ya Vikindu Mkoani Pwani kutokana na kutekeleza shughuli zake kinyume na taratibu za kimazingira.

Akizungumza mara baada ya timu ya wataalamu wa Mazingira kutoka NEMC kukagua kiwanda hicho, Meneja Utekelezaji wa Sheria (NEMC) Mhandisi Luhuvilo Mwamila ameeleza changamoto zilizobainika katika kiwanda hicho ikiwa ni Pamoja kuanzisha kiwanda bila kufanya Tathmini ya Athari kwa Mazingira (TAM) na kutokuwa na cheti cha Mazingira, kuanzisha kiwanda katikati ya makazi ya watu hivyo kuhatarisha usalama wa wakazi wa maeneo hayo, pia kukosa teknolojia madhubuti ya kudhibiti hewa ya kemikali inayosababishwa na uendeshaji wa kiwanda hicho, kukosekana kwa vifaa kinga kwa wafanyakazi na utiririshaji wa maji taka kwenye makazi ya watu bila kuyatibu.

Ameeleza kuwa, awali NEMC ilikagua kiwanda hicho na kutoa maelekezo ambayo kiwanda hicho kinatakiwa kuzingatia lakini hakikutekeleza maagizo hayo hivyo Baraza limechukua hatua ya kukifungia kiwanda hicho mpaka kitakapo tekeleza maelekezo yote yaliyotolewa na NEMC.

Ameongeza kuwa NEMC inaunga mkono uwekezaji nchini kwa kuwataka wawekezaji wote kufuata taratibu zote za Kimazingira zinazotolewa na NEMC zikiwemo kufanya Tathmini ya Athari kwa Mazingira na kupatiwa cheti Cha Mazingira.

Kwa upande wake, Kaimu Meneja wa Kanda ya Mashariki Kusini (NEMC) Bw. Noel Kikwale amezitaka Mamlaka zinazohisika na Mipango miji kutenga Maeneo maalumu ya viwanda na kuhakikisha wawekezaji wanafanya shughuli zao katika Maeneo hayo ili kuepuka changamoto za kimazingira na afya ya wananchi.

Ukaguzi huo ulihusisha wataalamu wa Mazingira kutoka NEMC wakiongozwa na Meneja wa Utekelezaji wa Sheria Mhandisi Bi. Luvilo Mwamila na Viongozi wa Kata ya Vikindu na wa Serikali za mitaa.






Na Mwandishi Wetu,Zanzibar

Waziri wa Kilimo, Umwagiliaji, Maliasili na Mifugo Zanzibar, Mhe. Suleiman Masoud Makame, amelishukuru Wakala wa Kimataifa wa Nguvu za Atomiki Duniani (IAEA) kwa namna shirika hilo linavyoisaidia Zanzibar katika sekta ya kilimo na mifugo.

Akizungumza katika ofisi za Wizara ya Kilimo Zanzibar baada ya kupokea ugeni kutoka IAEA, ugeni ulioongozwa na Bwana Gashaw Gebeyehu Wolde, Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kiufundi kwa Afrika, pamoja na Bi. Azza Kashlan, Afisa wa Usimamizi wa Programu, Waziri Makame alisema wizara yake itaendelea kushirikiana kwa karibu na IAEA ili kuhakikisha ushirikiano huo unaimarika zaidi, kama ambavyo umefanikiwa katika maeneo ya mazao na mifugo.

Kwa upande wake, Bwana Gashaw Gebeyehu Wolde alisema kuwa IAEA ina miradi ya kitaifa nchini Tanzania katika sekta ya kilimo, na nia yao ni kuona miradi hiyo inaleta matokeo chanya kwa wananchi.

Naye Prof. Najat Kassim Mohammed, Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Nguvu za Atomiki Tanzania (TAEC), alieleza kuwa kulikuwa na mradi wa kilimo uliomalizika mwaka jana, na kikao kilichofanyika Zanzibar kitasaidia kufanikisha tafiti mpya zitakazosaidia kupambana na wadudu wanaoshambulia matunda, jambo litakalowaletea wananchi maendeleo ya moja kwa moja.

Ziara hiyo ilionyesha dhamira ya IAEA ya kuendeleza ushirikiano wake na Zanzibar, hususan katika sekta za kilimo na mifugo, ili kuongeza usalama wa chakula, kuboresha maisha ya wananchi, na kuimarisha maendeleo endelevu visiwani.



 

Mwakilishi wa Katibu Tawala wa Mkoa wa Shinyanga Bw. David Lyamongi,akizungumza wakati wa semina ya kuwajengea uelewa kuhusu masuala ya ushindani wa kibiashara wadau na wafanyabiashara wa mkoa wa Shinyanga iliyofanyika  katika Ukumbi wa Makindo, Shinyanga.

Na.Mwandishi Wetu-SHINYANGA

Baraza la Ushindani, kwa niaba ya Mwenyekiti wake, Mhe. Jaji Rose Ally Ebrahimu, limewashukuru wadau na wafanyabiashara wa Mkoa wa Shinyanga kwa kujitokeza kwa wingi kushiriki katika semina ya kuwajengea uwezo iliyofanyika  katika Ukumbi wa Makindo, Shinyanga.

Semina hiyo imelenga kuwaongezea wadau uelewa kuhusu masuala ya ushindani wa kibiashara, haki zao kama wafanyabiashara pamoja na taratibu za kuwasilisha rufaa endapo hawataridhishwa na maamuzi ya mamlaka za udhibiti.

Akifungua semina hiyo, Bw. David Lyamongi, aliyemwakilisha Katibu Tawala wa Mkoa wa Shinyanga, CP Salumu Hamduni, aliwataka wadau na wafanyabiashara kutumia vyema fursa hiyo ya kujifunza ili kuimarisha shughuli zao za kibiashara.

Aidha, aliishukuru Baraza la Ushindani kwa kuwaletea wakazi wa Shinyanga elimu muhimu inayolenga kulinda haki zao katika biashara na kuimarisha ushindani wa haki katika soko.

Akizungumza katika semina hiyo, Msajili wa Baraza la Ushindani, Mhe. Mbegu Kaskasi, alisema kuwa Baraza la Ushindani ni chombo cha Serikali kilichoanzishwa kwa lengo la kusikiliza na kutatua migogoro ya ushindani wa kibiashara. Alisisitiza kuwa Baraza linaendelea kutoa elimu kwa umma ili kuhakikisha wadau na wafanyabiashara wanalifahamu, kulifikia kwa urahisi na kulitumia ipasavyo wanapohitaji haki.

Kwa upande wake Mjasiriamali kutoka Mkoa wa Shinyanga , Bw. Dedani Rutazibwa,alipongeza Baraza la Ushindani kwa kuandaa semina hiyo ya kuwajengea uwezo wadau. Alisema kutokana na umuhimu wa chombo hicho, ameiomba Serikali kupitia Baraza la Ushindani kuendelea kutoa elimu kwa makundi mbalimbali katika ngazi tofauti, ili wafanyabiashara waweze kufahamu haki zao pamoja na mamlaka sahihi za kuwasilisha rufaa zinazotokana na maamuzi ya mamlaka za udhibiti na Tume ya Ushindani.

Naye  Mkazi wa Shinyanga Mwl. Zezema Nyangaki, alisema kuwa elimu aliyopata kupitia semina hiyo imemfungua macho, akieleza kuwa awali hakuwa na uelewa kuhusu uwepo wa mamlaka za udhibiti zinazopokea malalamiko ya wafanyabiashara. Aliongeza kuwa mafunzo hayo yamemsaidia kufahamu kuwa endapo hataridhishwa na maamuzi ya mamlaka hizo, anaweza kukata rufaa katika Baraza la Ushindani ili kupata haki yake kwa mujibu wa sheria.


Top News