Katika kuendeleza dhamira ya uwajibikaji kwa jamii, Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) limetembelea Kituo cha Watoto Yatima cha Umra Orphanage jijini Dar es Salaam, na kutoa msaada wa mahitaji muhimu sambamba na kuwapa faraja watoto wanaolelewa kituoni hapo, kuelekea sikukuu ya Idd.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Meneja wa Masoko na Mahusiano ya Umma wa STAMICO, Deus Alex , amesema lengo la watumishi wa shirika hilo ni kushiriki na jamii kwa vitendo, hususan kwa makundi yenye uhitaji maalum.

Amesema msaada huo haujalenga tu kukidhi mahitaji ya msingi, bali pia kuwajengea watoto hao imani, matumaini na ujasiri wa kuamini katika ndoto zao licha ya changamoto wanazokutana nazo.

“Tumekuja hapa si kwa ajili ya kutoa mahitaji pekee, bali pia kuwa karibu na watoto hawa, kuwapa moyo na kuwahakikishia kuwa wana uwezo wa kufikia mafanikio makubwa katika maisha yao,” amesema Mtukamazina.

Ameongeza kuwa, STAMICO itaendelea kutambua na kushirikiana na jamii inayowazunguka, kama sehemu ya mchango wake katika kujenga taifa lenye mshikamano na ustawi wa pamoja.

Kwa upande wake, Katibu wa Umra Orphanage Center, Hamza Ahmed Kanyange, amepongeza hatua hiyo akisema msaada uliotolewa umefika kwa wakati muafaka na umeleta faraja kubwa kwa watoto pamoja na walezi wao.

Amesema ujio wa STAMICO umeongeza furaha na kuwapa watoto motisha mpya, huku akibainisha kuwa vituo vya aina hiyo bado vinakabiliwa na changamoto mbalimbali zinazohitaji ushirikiano wa wadau.

Aidha, ametoa wito kwa taasisi, makampuni na watu binafsi kuendelea kujitokeza kusaidia makundi yenye mahitaji maalum, ili kuhakikisha wanapata huduma bora na maisha yenye matumaini.



















NA EMMANUEL MBATILO, BAGAMOYO

WIZARA ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kupitia Wakala wa Maendeleo ya Uongozi wa Elimu (ADEM) itaendelea kutoa fursa za mafunzo endelevu ya viongozi wa elimu wa ngazi mbalimbali na wadau wengine wa elimu ili waweze kuimarisha uongozi, usimamizi na uendeshaji wa shule kwa ajili ya utoaji wa elimu bora nchini.

Ameyasema hayo Mkurugenzi wa Elimu msingi, Abdul Maulid wakati akimwakilisha Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Wanu Hafidh Ameir katika ufungaji mafunzo ya uongozi, usimamizi na utawala bora wa elimu kwa Maafisa Elimu Kata Tanzania Bara yaliyofanyika katika Wakala wa Maendeleo ya Uongozi wa Elimu (ADEM), katika Halmashauri ya Bagamoyo, mkoani Pwani.

Amesema mafunzo hayo yamekusudiwa kuwajengea uwezo viongozi na wasimamizi wa taasisi za elimu ili waweze kusimamia ipasavyo rasilimali na michakato ya utoaji wa elimu, huku wakizingatia misingi ya uongozi bora, uwazi na uwajibikaji.

"Ni matumaini yetu kuwa, ADEM mtaendelea kutoa mafunzo yanayoelenga kuimarisha uongozi, usimamizi na uendeshaji wa elimu kwa njia endelevu na yenye mafanikio pamoja na kufanya tafiti mbalimbali zakielimu na kutoa ushauri wa kitaalam katika masuala ya uongozi. Ninawasihi muendelee kufanya kazi kwa weledi ili kutimiza malengo ya kuanzishwa kwa ADEM". Amesema

Ameongeza kuwa ushirikishwaji wa jamii, matumizi sahihi ya takwimu za elimu na utoaji wa fursa za mafunzo endelevu kwa walimu ni mambo muhimu katika kuimarisha ubora wa elimu.

Ametoa wito kwa washiriki wa mafunzo hayo kutumia maarifa waliyoyapata kuboresha utendaji wao, akisisitiza umuhimu wa kufanya kazi kwa weledi, ubunifu, kujituma na uzalendo ili kufanikisha malengo ya sekta ya elimu nchini.

Kwa upande wake Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Maendeleo ya Uongozi wa Elimu (ADEM), Dkt. Maulid J. Maulid amesema kuwa mafunzo hayo yametekelezwa kama sehemu ya utekelezaji wa dhamira ya Serikali ya kuimarisha mifumo ya usimamizi wa elimu kwa kuzingatia misingi ya uongozi bora, uwajibikaji na ufanisi katika utoaji wa huduma za elimu.

"Mpango huu ulianza kwa kutoa mafunzo ya kuwajengea uwezo Walimu Wakuu wa shule za msingi kuhusu Uongozi, Usimamizi na Utawala Bora wa Elimu, yaliyowahusisha Walimu Wakuu 17,817 kutoka Mikoa yote 26 ya Tanzania Bara". Amesema

Amesema kuwa mafunzo hayo yamelenga kuwaimarisha Walimu Wakuu katika kusimamia shule kwa kutumia mbinu stahiki za uongozi pamoja na kuzingatia sera, miongozo na viwango vya kitaifa ili kuhakikisha kuwa shughuli za ufundishaji na ujifunzaji zinafanyika kwa ubora, ufanisi na kwa kuzingatia viwango vinavyokubalika kitaifa na kimataifa.

Pamoja na hayo Dkt. Maulid amesema kuwa tathmini inaonyesha kiwango kikubwa cha mabadiliko ya kiutendaji kwa walimu wakuu katika kuongoza na kusimamia shule zao baada ya kupatiwa mafunzo hayo.

`














Na Mwandishi Wetu, London

Waziri wa Afya, Mhe. Mohamed Mchengerwa, ametangaza kuwa Tanzania iko tayari kushirikiana na wawekezaji wa kimataifa katika kukuza Sekta ya Afya na Sayansi , akisisitiza kuwa taifa linaelekea kuwa kitovu cha uzalishaji wa dawa na bidhaa za afya barani Afrika.

Akizungumza leo jijini London kwa niaba ya Waziri Mchengerwa kwenye Jukwaa la Uwekezaji la Afya na Sayansi ikiwa ni jitihada za Serikali za kuleta mageuzi makubwa katika uwekezaji wa viwanda vya ndani vya uzalishaji wa bidhaa za afya na vifaa tiba Naibu Katibu Mkuu anayeshughulikia eneo la Dawa na vifaaa tiba Emmanuel Tayari amewahakikishia wawekezaji dhamira ya dhati ya Serikali ya kuweka mazingira rafiki na wezeshi kwa wawekezaji kufanya uwekezaji wa viwanda vya dawa na vifaa Tiba nchini Tanzania.


Jukwaa hiyo limeratibiwa na Ubalozi wa Tanzania nchini Uingereza na Wizara ya Afya ambapo Mhe. Balozi Mbelwa Kairuki na upande wa Wizara Dkt. Seif A. Shekalaghe, Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Emmanuel Tayari Naibu Katibu Mkuu anayesimamia Dawa na Vifaa Tiba, Dkt. Grace Magembe Mganga Mkuu wa Serikali wamehudhuria. Aidha, wwngine ni Watendaji kutoka TISEZA, TMDA, MSD, MUHAS pamoja na wataalam wa Kikosi Kazi cha Kuharakisha Uwekezaji wa Dawa (PIAT) nchini.


Alibainisha kuwa juhudi hizo zinaungwa mkono kikamilifu na Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, ambaye anaipa kipaumbele ajenda ya uwekezaji katika afya kama sehemu ya kuimarisha usalama wa afya, maendeleo ya viwanda na ushirikiano wa kimkakati.


Katika hotuba yake, Mchengerwa alieleza kuwa Tanzania sasa inaiona sekta ya afya si tu kama huduma ya kijamii, bali pia kama injini ya ukuaji wa uchumi. “Tunataka kuwa zaidi ya soko la bidhaa za afya zinazoagizwa kutoka nje. Tunataka kuwa kitovu cha uzalishaji, ubunifu na usambazaji wa kikanda,” alisema.

Alisisitiza kuwa uzoefu wa janga la UVIKO-19 umeonesha umuhimu wa nchi kuwa na uwezo wa ndani wa kuzalisha dawa, chanjo na vifaa tiba, akionya kuwa utegemezi mkubwa wa uagizaji kutoka nje unaweza kuhatarisha upatikanaji wa huduma muhimu wakati wa dharura.

Kwa mujibu wa Waziri huyo, Tanzania imeweka mazingira rafiki kwa uwekezaji, ikiwa ni pamoja na uthabiti wa uchumi, idadi kubwa ya watu zaidi ya milioni 65, na mageuzi ya mfumo wa bima ya afya yatakayosaidia kuongeza mahitaji ya huduma za afya kwa utaratibu unaotabirika.

Aliongeza kuwa nafasi ya Tanzania katika Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) inaipa nchi faida ya kipekee ya kuhudumia soko kubwa la kikanda, jambo linalovutia zaidi wawekezaji.

Katika hatua ya kuimarisha sekta hiyo, serikali inaendelea kuendeleza Eneo Maalum la Kiuchumi la Dawa la Mloganzila pamoja na vituo vya uzalishaji wa dawa katika maeneo ya Mloganzila na Kibaha. Pia imeanzisha Kikosi Kazi cha Kuharakisha Uwekezaji wa Dawa (PIAT) kwa lengo la kurahisisha taratibu na kuharakisha uwekezaji wa kimkakati.



Mchengerwa alisisitiza kuwa Tanzania haitaki kuwa soko la teknolojia zilizopitwa na wakati au bidhaa duni, bali inalenga uzalishaji wa dawa za kisasa zinazokidhi viwango vya kimataifa. “Dawa duni hugharimu maisha. Hatuwezi kuendelea kuwa soko la dawa za jana wakati dunia imeendelea,” alionya.

Alihimiza wawekezaji kuangalia fursa zilizopo katika uzalishaji wa dawa, vifaa tiba, uchunguzi wa magonjwa, mifumo ya usambazaji, pamoja na utafiti na maendeleo ya rasilimali watu.

Kwa upande wake, alisema Uingereza ina nafasi muhimu katika kushirikiana na Tanzania kutokana na uzoefu wake katika teknolojia ya afya, utafiti na uwekezaji, akikaribisha ubia wa kimkakati utakaosaidia kukuza sekta hiyo.



Akihitimisha, Waziri Mchengerwa alitoa wito kwa wawekezaji wa kimataifa kuchangamkia fursa zilizopo nchini Tanzania, akisisitiza kuwa serikali iko tayari kuwezesha mazingira bora ya uwekezaji.

“Fursa ipo, soko linakua, na dhamira ni thabiti. Tunakaribisha wawekezaji kushirikiana nasi kujenga mustakabali wa afya barani Afrika,” alisema.

Katika Jukwaa hilo pia Meneja wa Biashara na Maendeleo, Philip Conradi wa Kampuni kubwa Duniani ya uzalishaji wa Bidhaa za Afya- Sartorius alihudhuria.






 



Na Oscar Assenga,TANGA

KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Maji na Mazingira wametembelea maendeleo ya utekelezaji wa mradi wa Maji wa Hatifungani ya Kijani (Green Bond) wenye thamani ya Sh.Bilioni 53.3 unaolenga kuboresha hali ya upatikanaji wa huduma kwa wakazi wa Jiji la Tanga na wilaya za karibu

Akizungumza wakati wa ziara ya kukagua miradi inayotekelezwa na Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Tanga (Tanga UWASA) Machi 17,2026 Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Jackson Kiswaga alisema kwamba wameridhishwa na utekelezaji wa mradi huo



Mradi huo kwa sasa umefikia asilimia 65 ya utekelezaji wake na unatarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Octoba mwaka huu ambao utakuwa mkombozi mkubwa kwa wananchi.

“Kwa kweli tumetembelea mradi huu na tumeona namna unavyotekelezwa na kumeridhishwa nao kazi nzuri inaendelea “Alisema

Katika hatua nyengine Mwenyekiti wa Kamati hiyo alimpongeza Rais Dkt. Samia Suluhu kwa kuruhusu ushiriki wa sekta binafsi katika uzalishaji wa maji.

Aidha pia aliitaka Wizara ya Maji kuhakikisha wakandarasi wanalipwa kwa wakati ili wasikwamishe kasi ya ujenzi wake

Aliongeza kwamba wanamshukuru Rais kwa kutoa kiasi cha Bilionio 35 kwa ajili ya mradi wa Mkinga-Horohoro kupitia fedha za ndani.


Alisema Kamati hiyo inataka kuona mradi huu unakamilika kwa wakati ili ifikapo mwaka 2030 malengo ya Serikali ya kufikisha maji kwa asilimia 100 yawe yametimia.


Kwa upande wake Mkurugenzi wa Tanga UWASA, Mhandisi Godfrey Hilly alisema kuwa mradi huo unajumuisha upanuzi wa kituo cha kusukuma maji cha Mabayani kutoka lita milioni 42 hadi milioni 72 kwa siku, na ukarabati wa mtambo wa Mowe utakaofikisha uzalishaji wa lita milioni 60 kwa siku.

Hata hivyo Meneja wa RUWASA Mkoa wa Tanga, Mhandisi Upendo Lugongo alisema mkoa unafikia asilimia 79 ya upatikanaji wa maji,.



Alisema kwa wilaya ya ya Mkinga wakitarajiwa kupanda kutoka asilimia 72.1 hadi 89.03 mara baada ya mradi wa Mkinga-Horohoro kukamilika wenye thamani ya shilingi bilioni 35 utakapokamilika.

Kamati ya Bunge imekagua maendeleo ya utekelezaji wa mradi huo ambao katika awamu yake ya kwanza unatarajiwa kuhudumia jumla ya vijiji 17 ndani ya wilaya hiyo.

Mhandisi Upendo alisema mradi huo kwa ujumla umefikia asilimia 65 ya utekelezaji wake. Katika ziara hiyo, Kamati imezindua rasmi upatikanaji wa maji katika Kata ya Mtimbwani, ambapo wananchi wa eneo hilo sasa wameanza kupata huduma ya maji safi ya bomba, ikiwa ni sehemu ya mafanikio ya awali ya mradi huo mkubwa utakaohudumia vijiji 37 utakapokamilika kikamilifu.

Awali akizungumza Waziri wa Maji, Mhe. Jumaa Aweso, alimpongeza mkandarasi wa STC huku akieleza kwamba Serikali itaendelea kusimamia ubora wa huduma na kuwashirikisha watu binafsi katika usambazaji ili kuwafikia wananchi wa vijijini haraka zaidi.

Hata hivyo Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo Pius Lyanda, aliishauri Serikali kutenga bajeti maalumu kwa ajili ya kuhifadhi vyanzo vya maji na bwawa la Mabayani ili kuzuia uharibifu wa mazingira unaotokana na shughuli za kibinadamu.






Top News