Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo imeiagiza Wakala wa Vipimo (WMA) kuongeza nguvu katika kudhibiti usahihi wa vipimo ili kuhakikisha huduma wanazopata wananchi zinaendana na thamani halisi ya fedha wanayotumia

Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa Kamati ya kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo Mhe. Deodatus Mwanyika (Mb), Wakati Kamati hiyo ili pokea Taarifa ya Wizara ya Viwanda na Biashara kuhusu utekelezaji ya Miradi ya Maendeleo kwa mwaka 2025/26 kutoka Wakala wa Vipimo (WMA) na Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE) Taasisi zake yake Machi 10, 2026 , Bungeni jijini Dodoma.

Mwanyika amesisitiza kuwa vita dhidi ya lumbesa haipaswi kuachiwa WMA pekee, bali inahitaji nguvu ya pamoja kati ya Halmashauri, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), na Serikali Kuu ili kufanya oparesheni za nchi nzima.

Nao, Wajumbe wa Kamati hiyo walizipongeza WMA na CBE kwa utekelezaji wa miradi mbalimbali na kutoa maoni na mapendekezo mbalimbali yaliyolenga kuboresha utekelezaji wa Miradi hiyo kwa ufanisi.

Naye, Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Dennis Londo (Mb), alifafanua kuwa msingi wa Tanzania ya Viwanda ni kilimo ambapo WMA inatekeleza jukumu la kumlinda mkulima, huku akibainisha kuwa idadi kubwa ya watumishi wa Wakala huyo wanazalishwa na Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE), jambo linaloashiria kuwepo kwa uhusiano mkubwa wa kikazi baina ya taasisi hizo mbili.

Naye Afisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Vipimo (WMA), Bw. Alban Kihulla, amesema kuwa taasisi hiyo, kwa wakishirikiana na mamlaka nyingine za Serikali pamoja na sekta binafsi, wanaenda kupata suluhisho la kudumu la malalamiko ya wananchi ambayo yamekuwa yakiwasilishwa kwa muda mrefu kuhusu ukosefu wa usahihi wa vipimo katika maeneo mbalimbali ikiwemo lumbesa.

Kwa upande wake Mkuu wa Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE), Prof. Edda Lwoga amesema miradi ya majengo inayojengwa kwenye Kampasi mbalimbali za Chuo hicho mara itakapokamilika itaboresha mazingira ya kujifunzia na kuongeza udahili wa wanafunzi katika chuo hicho.


NA FARIDA MANGUBE, MOROGORO 

Kampeni ya "Soma na Mkarafuu," inayotekelezwa na Serikali ya Mkoa wa Morogoro, inatoa fursa mpya ya kiuchumi kwa wanafunzi wa kidato cha kwanza Baada ya kuwapatia miche kumi ya  mkarafuu. 

Kampeni hii, ambayo inalenga kukuza kilimo cha zao la mkarafuu, inawapa wanafunzi na familia zao njia ya kujitegemea kifedha baada ya miaka minne, wakati ambapo zao hilo linapozalisha.


KILIMO CHA MKARAFUU NA FAIDA ZAKE KIMATAIFA

Mkarafuu ni zao lenye soko kubwa duniani, na linapandwa katika maeneo mbalimbali duniani kwa faida yake kubwa kiuchumi, kwa mujibu wa Katibu Tawala wa Mkoa wa Morogoro, Musa Ali Musa, kila mkarafuu unazaa kilo tano na kuendelea na kilo moja inauzwa kati ya shilingi 15,000 hadi 20,000. 

"Miche ya mkarafuu inakua kwa kasi na inaanza kutoa mazao wakati mwanafunzi anapomaliza mtihani wa kidato cha nne, hivyo atakuwa na uwezo wa kujimudu kifedha akiwa katika kidato cha tano au anapojiunga na mafunzo ya ufundi," alisema Musa.

Kampeni hii ni muhimu si tu kwa kuongeza kipato kwa wanafunzi na familia zao, bali pia inahamasisha wanafunzi kufanya bidii katika masomo yao kwa kuwa wanajua kuwa wataweza kujimudu kifedha kupitia kilimo cha mkarafuu baada ya kumaliza masomo.

 Wanafunzi watakuwa na uhuru wa kuchagua ni njia gani ya maisha wanayotaka, bila kuathiriwa na changamoto za kifedha.


KUPUNGUZA NDOA ZA MAPEMA NA UTORO KWA WATOTO WA KIKE

Kampeni hii pia ina mchango mkubwa katika kupunguza utoro na ndoa za mapema, hasa kwa watoto wa kike. Kwa kuwa watoto wa kike sasa watakuwa na fursa ya kujitegemea kifedha, watakuwa na uwezo wa kugharamia masomo yao na kujiendeleza kimasomo, jambo ambalo linawapa uhuru zaidi wa kuchagua mustakabali wao. 

"Watoto wa kike, ambao mara nyingi walikosa fursa ya kujitegemea kutokana na ukosefu wa fedha, sasa watakuwa na njia ya kujimudu," aliongeza Katibu Tawala.

Fatuma Amri, mwanafunzi wa Shule ya Sekondari Tawa, ameeleza furaha yake kuhusu mpango huu wa kipekee, akisema, "Hii itatufanya tusome kwa bidii na kuwa na uhakika wa kuendelea na masomo yetu baada ya kidato cha nne. Hatuwezi tena kuwa na wasiwasi kuhusu ada na gharama za shule."

MAFAKIO YA KAMPENI NA MATUMAINI YA BAADAYE

Kampeni ya "Soma na Mkarafuu" inaonyesha mafanikio ya awali, na kwa mwaka 2026, jumla ya miche 2,650 ya kokoa iligawiwa kwa wanafunzi wa Halmashauri ya Mlimba, na miche 9,680 imetolewa kwa wanafunzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Morogoro.

 Miche hii ya kilimo itasaidia wanafunzi kujiendeleza kimasomo na kiuchumi baada ya kumaliza kidato cha nne.

Dkt. Rozalia Rwegasira, Katibu Tawala Msaidizi Sehemu ya Uchumi na Uzalishaji Mali, anasema kuwa kampeni hii itasaidia kuinua uchumi wa familia na pia itawawezesha wanafunzi kuanzisha miradi ya kilimo itakayowaingizia kipato.

 "Miche ya mkarafuu itachangia katika kukuza uchumi wa wanafunzi na familia zao, na itakuwa na manufaa makubwa kwa mkoa na taifa kwa ujumla," alisema Dkt. Rwegasira.

MOTISHA KWA WANAJUMUIYA BORA

Serikali ya Mkoa wa Morogoro pia imeandaa motisha kwa wanafunzi watakaofanya vizuri katika utunzaji wa miche ya mkarafuu. Wanafunzi watakaofanya vizuri watajipatia zawadi za sare za shule, madaftari, na zawadi kubwa ya safari ya kwenda Zanzibar kwa mwanafunzi atakayefanya vizuri zaidi.








Wanawake watumishi wa Mamlaka  Hifadhi ya Ngorongoro katika muendelezo wa  kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani, wamedhihirisha kwamba mchawi wa mwanamke si mwanamke  kwa kutembelea  shule ya Sekondari ya wasichana Ngorongoro na kuwapa tabasamu la  msaada wa vifaa mbalimbali

Akiongea kwa Niaba ya Kamishna wa Uhifadhi, Afisa Uhifadhi Mkuu Sarah Lushu ameeleza kuwa vitu ambavyo Mamlaka vinajumuisha vyakula, Sabuni, vifaa vya kujifunzia, taulo la kike, Vyombo vya kuogea, kupikia na kufulia na mahitaji mbalimbali mahususi kwa wanafunzi wanawake ilo kuwaongezea tabasabu na kuonyesha nguvu ya mwanamke katika Jamii.

"Msaada huu ni sehemu ya jitihada za Shirika kupitia kamishna wa Uhifadhi kuimarisha uhusiano na jamii iliyopo ndani ya Hifadhi na kuhakikisha kuwa wanafunzi hasa wa kike wanapata mahitaji muhimu ya kuwapa utulivu wa kusoma na kupata ufaulu mzuri" alifafanua PCO Sarah.

Msaada huu unadhihirisha wazi kuwa wanawake ni watu wa kusaidiana na mchawi wa mwanamke sio Mwanamke. 






Na Hassan Kimweri, WAF - Dar es Salaam

Mganga Mkuu wa Serikali Dkt. Grace Magembe amewataka waajiri kuhakikisha kila muajiriwa anakuwa na uhakika wa matibabu kuelekea utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote na Dira ya Maendeleo ya Taifa ya mwaka 2050.

Dkt. Magembe amesema hayo leo Machi 10, 2026 baada ya wasilisho la maandalizi ya Bima ya Afya kwa Wote kwenye mkutano na Wakurugenzi Wakuu wa Makampuni ya Tanzania (CEO Roundtable of Tanzania – CEOrt) uliofanyika jijini Dar es Salaam na kuwakutanisha viongozi kutoka serikalini, sekta binafsi na washirika wa maendeleo.

"Serikali inaendelea kuimarisha utekelezaji wa mpango wa Bima ya Afya kwa Wote kwa kuwa na ubunifu wa vyanzo vya fedha pamoja na kuanzisha kitita muhimu kitakachohakikisha kila mwananchi anapata huduma muhimu za afya katika vituo vyote vya kutolea huduma nchini," amesema Dkt. Magembe

Aidha, Dkt. Magembe amesema Serikali imeanza utekelezaji wa Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote ambapo utekelezaji wake unafanyika kwa awamu, awamu ya kwanza ilianza Januari 6, 2025 kwa kuwatambua zaidi ya familia milioni 3.6 kidijitali kwa kushirikiana na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) pamoja na Mamlaka za Serikali za Mitaa," amesema Dkt. Magembe

Katika hatua nyingine, Dkt. Magembe amesema Serikali imeanzisha Mfuko wa kugharamia huduma za Afya (Health Equity Fund) utakaosaidia kugharamia huduma za afya kwa wananchi wasio na uwezo wa kumudu gharama za matibabu kupitia vyanzo mbalimbali.

Pia, amesema Serikali imeanza kuchukua hatua za kupunguza utegemezi wa misaada ya wahisani katika sekta ya afya kwa kuimarisha zaidi vyanzo vya ndani vya fedha na kutafuta mbinu mpya za ubunifu zitakazochangia kugharamia huduma za afya nchini.

Hata hivyo, ameeleza dhamira ya Serikali kuimarisha viwanda vya ndani vya dawa na bidhaa za afya ili kuhakikisha upatikanaji wa dawa unakuwa wa uhakika, kuongeza ajira na kukuza sekta binafsi kuelekea utekelezaji wa bima ya afya kwa wote.

Mwisho, Serikali imewahimiza wawekezaji kutumia fursa zilizopo katika sekta hiyo, huku ikiendelea kukuza ushirikiano kati ya sekta ya umma na binafsi katika uzalishaji wa dawa na vifaa tiba nchini.










-Asema Serikali haitavumilia uzembe katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba ameiagiza Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kufanya uchunguzi wa kina kuhusu makadirio na matumizi ya fedha za ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Kalambo mkoani Rukwa.

Ametoa agizo hilo leo Jumanne (Machi 10, 2026) wakati akizungumza na wananchi wa Kasanga, Wilaya ya Kalambo mkoani Rukwa baada ya kupokea taarifa ya maendeleo ya ujenzi wa hospitali hiyo, ambapo baadhi ya majengo bado hayajakamilika licha ya fedha kutolewa na Serikali.

Serikali ilitoa zaidi ya Sh. bilioni 4 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Kalambo ambapo katika awamu ya kwanza majengo saba ya huduma za afya yalijengwa, ikiwemo jengo la wagonjwa wa nje (OPD), jengo la mama na mtoto, maabara, duka la dawa pamoja na miundombinu mingine ya huduma za hospitali. Hata hivyo, licha ya fedha hizo kutolewa na baadhi ya majengo kukamilika, majengo mawili muhimu ambayo ni jengo la theatre (chumba cha upasuaji) na wodi ya wanaume hayajakamilika.

Akizungumzia utekelezaji wa mradi huo, Waziri Mkuu ameonesha kutoridhishwa na taarifa ya kuchelewa kukamilika kwa baadhi ya majengo ya hospitali hiyo.

“Ninyi mmeomba fedha, hamjapunguziwa hata senti moja ya fedha mlizoomba, mmepewa. Halafu mnapofika kwenye utekelezaji mnasema fedha haitoshi. Hii si sawa,” amesema.

Kutokana na hali hiyo, Dkt. Mwigulu amemtaka Kamanda wa TAKUKURU mkoa wa Rukwa Bw. Mzalendo Widege kufanya uchunguzi wa kina ili kubaini kama kulikuwa na uzembe au udanganyifu katika makadirio na matumizi ya fedha za ujenzi wa majengo ya hospitali hiyo.

“Kamanda wa TAKUKURU nenda kachunguze, angalia kama kweli makadirio yalikuwa sahihi au kuna jambo lingine limejificha. Nipate taarifa ili tuweze kuchukua hatua stahiki,” amesema.

Waziri Mkuu amesema Serikali haitavumilia uzembe, ubadhirifu au ukiukwaji wa maadili katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwa kuwa fedha zinazotolewa ni mali ya umma na zinapaswa kutumika kwa manufaa ya wananchi.

Aidha, amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan imefanya uwekezaji mkubwa katika sekta ya afya ili kuboresha huduma za matibabu nchini.

Amesema katika kipindi cha takribani miaka minne, Serikali imejenga vituo vya afya zaidi ya 649 na zahanati zaidi ya 2,800 ili kusogeza huduma za afya karibu na wananchi.

Pia Serikali imenunua vifaa vya kisasa vya uchunguzi wa magonjwa ikiwemo mashine za MRI katika hospitali za rufaa na CT Scan katika hospitali za mikoa.


Aidha, wataalamu zaidi ya 5,000 wa sekta ya afya wameajiriwa ndani ya siku 100 kama alivyoahidi Rais wakati wa kampeni za uchaguzi.






 

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba leo Jumanne (Machi 10, 2026) amekagua miundombinu na utendaji kazi wa Bandari ya Kasanga iliyopo Wilaya ya Kalambo mkoani Rukwa, akiwa katika ziara yake ya kikazi mkoani humo.

TPA ilifanya upanuzi wa bandari ya Kasanga mwaka 2019 kwa kuongeza urefu wa gati kutoka mita 20 hadi 120 ya kina cha mita 14 pamoja na ujenzi wa nyumba za wafanyakazi na jengo la kuhudumia abiria 200 kwa wakati mmoja kwa gharama ya shilingi bilioni 4.7. Pia kumejengwa maghala mawili ya kuhifadhi mizigo yenye uwezo wa tani 2,500 kila moja.

Katika kipindi cha Julai 2023 hadi Desemba 2025, bandari hiyo imehudumia jumla ya tani 3,418 za mizigo, abiria 3,648, meli 11 pamoja na maboti 337. Miongoni mwa mizigo inayohudumiwa katika bandari hiyo ni saruji, makaa ya mawe pamoja na mazao ya chakula kama mahindi, mchele na unga wa sembe.

Bandari hiyo ni miongoni mwa miundombinu ya kimkakati inayochochea shughuli za usafirishaji na biashara katika ukanda wa Ziwa Tanganyika na kuchangia ukuaji wa uchumi wa Mkoa wa Rukwa na maeneo jirani.



 

Na Hassan Kimweri, WAF - Dar es Salaam

Serikali kupitia Wizara ya Afya kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo katika Sekta ya Afya, inaendelea kujidhatiti kwa kuimarisha mifumo ya huduma za afya kupitia tafiti mbalimbali ili kuhakikisha wagonjwa wenye magonjwa adimu wanapata huduma stahiki kwa wakati.

Hayo yamesemwa leo Machi 4, 2026 na Mganga Mkuu wa Serikali Dkt. Grace Magembe wakati akifungua Kongamano la 16 la kusambaza matokeo ya tafiti za magonjwa adimu lililofanyika Muhimbili University of Health and Allied Sciences (MUHAS) jijini Dar es Salaam.

"Serikali inayapa uzito stahiki magonjwa haya adimu, ili tuweze kuyashughulikia kwa kina na upana wake, kwa kushirikiana na Taasisi kama Ali Kimara, sekta mashirika na sekta binafsi tutawafikia watoto wengi zaidi," amesema Dkt. Magembe.

Aidha, Dkt. Magembe amesema hadi kufikia Desemba mwaka 2025 zaidi ya wataalamu wa afya 200 katika vituo 14 walikuwa wamepatiwa mafunzo ya kuanzisha vitengo vya tiba ya magonjwa adimu ikiwemo 'hemofilia' kuanzia ngazi ya msingi.

"Serikali imeshachukua hatua za kujenga uwezo wa maabara yetu ya Taifa, mafunzo kwa wataalamu wa Afya na kuanzisha vitengo maalum vya matibabu ya magonjwa adimu kuanzia ngazi ya msingi (Zahanati, kituo cha afya na hospitali za wilaya), tulianza na Seli mundu (Sickle cell) na sasa Hemofilia ambapo tayari wagonjwa 500 wamegundulika na wanaendelea na tiba,” amesema Dkt. Magembe.

Pia, katika Kongamano hilo Dkt. Magembe amewataka wataalamu hao wa tafiti wakiwemo MUHAS na NIMR kujadilina kwa kina na kwa uwazi kujua mafaniko, changamoto na kutoa mapendekezo na kuyawasilisha Serikalini yaweze kufanyiwa kazi.

Kongamano hilo limeandaliwa na Muhimbili University of Health and Allied Sciences (MUHAS) kwa kushirikiana na Taasisi ya Ali Kimara Rare Disease Foundation (AKRDF).





Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi ametoa wito kwa Wizara zinahusiana na Sekta ya Mazingira, kufanya kazi kwa ushirikiano ili kuwa na mpango wa pamoja utakaowezesha uhifadhi endelevu wa mazingira.

Makamu wa Rais ametoa wito huo, wakati akifanya mazungumzo na Waziri wa Maliasili na Utalii Dkt. Ashatu Kijaji, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhandisi Hamad Masauni, Naibu Waziri wa Maji, Mhandisi Kundo Mathew, Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Dkt. Festo Dugange, Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Dkt. Richard Muyungi pamoja na wataalamu kutoka Wizara hizo, katika kikao kilichofanyika mkoani Dodoma.

Amesema Wizara hizo zinategemea zaidi uhifadhi wa Mazingira, mathalani Wizara ya Maji itafanya kazi kwa ufanisi kama vyanzo vya maji havitaaribiwa, vilevile mpango wa matumizi ya nishati safi ya kupikia utawezesha kuokoa ukataji miti ovyo na hivyo kulinda misitu iliyopo.

Makamu wa Rais amewasihi Viongozi wa Wizara hizo, kuongeza jitihada ili kuifanya Tanzania kuwa mfano wa kuigwa katika kulinda na kuhifadhi mazingira kwa kuwa ina misitu ya kutosha pamoja na wataalamu wenye uwezo wa kufanikisha hilo.

Amesema tayari Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan alizindua mpango wa kukijanisha nchi, pamoja na kutoa hamasa za mara kwa mara za upandaji miti, ikiwemo kutumia siku yake ya kuzaliwa kuhamasisha upandaji miti kitaifa, hivyo ni vema watendaji wote kuongeza bidii katika kuhakikisha Tanzania inakua kinara wa uhifadhi wa mazingira.

Halikadhalika, Makamu wa Rais amewahimiza Viongozi hao, kuandaa mpango ambao utawezesha kukabiliana na changamoto za kuhifadhi miti baada ya kupandwa ili kuweza kufikia malengo yaliyokusudiwa.

Makamu wa Rais, ameipongeza Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kuwa na mpango wa upandaji miti Kitaifa ambao unakwenda sambamba na Siku ya Misitu Duniani.








Top News