Manyoni, Singida, Februari 12, 2026 — Ziara ya mafunzo ya wataalamu wa Idara ya Misitu Zanzibar imeingia siku ya pili leo kwa ujumbe huo kuanza rasmi mafunzo ya vitendo katika Shamba Darasa la Nyuki la TFS, wilayani Manyoni.

Mafunzo hayo yameanza kwa mada ya uanzishaji na usimamizi bora wa Hifadhi za Nyuki (Bee Reserves) iliyowasilishwa na Askari wa Uhifadhi – Ufugaji Nyuki Wilaya ya Manyoni, Jacline Leshabari, akieleza hatua za kisheria, kiutawala na kiikolojia zinazohitajika katika kuanzisha na kulinda maeneo maalum ya nyuki.

Akiwasilisha mada hiyo, Leshabari amesema hifadhi za nyuki zimekuwa nyenzo muhimu si tu katika kuongeza uzalishaji wa asali na mazao yatokanayo na nyuki, bali pia katika kulinda misitu na bioanuai. “Usimamizi madhubuti wa hifadhi hizi unahakikisha upatikanaji endelevu wa malighafi za nyuki huku ukihifadhi mfumo wa ikolojia,” amesema.

Kwa mujibu wa ratiba ya mafunzo, wataalamu hao kutoka Zanzibar wanatarajiwa pia kujionea kwa vitendo utambuzi wa maeneo ya hifadhi, uwekaji wa mizinga ya kisasa, pamoja na mbinu za kushirikisha jamii katika kulinda na kunufaika na rasilimali za nyuki.

Mkurugenzi wa Idara ya Misitu Zanzibar, Said Juma Ali, amesema mafunzo ya siku ya pili yamewapa mwanga mpana juu ya namna TFS inavyounganisha uhifadhi na uchumi wa jamii kupitia sekta ya nyuki. Amesisitiza kuwa uzoefu huo utasaidia Zanzibar katika mpango wake wa kuanzisha hifadhi za nyuki na kuendeleza utalii wa nyuki.

Ziara hiyo ya siku tano inatarajiwa kuendelea kwa mafunzo zaidi kuhusu uchakataji wa asali, viwango vya ubora na masoko, huku ushirikiano kati ya TFS na Idara ya Misitu Zanzibar ukitajwa kuwa kichocheo cha mageuzi ya sekta ya nyuki nchini.




 

Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Elimu Tanzania Dkt. Aneth Komba amesema, Serikali imetoa vitabu vya masomo ya Elimu ya Amali bure kwa shule zote za umma na binafsi ili kuongeza hamasa katika ufundishaji na ujifunzaji wa masomo hayo yatayosaidia kukabiliana na changamoto ya ajira kwa mwanafunzi pindi wanapohitimu.

Dkt. Komba amesema hayo leo Februari 12, 2026 katika zoezi la ugawaji wa vitabu vya Amali kwa wakuu wa shule zote Tanzania Bara ambazo zinatoa Elimu ya Sekondari katika mkondo huo.

Amesema, mwaka 2024 Serikali ilianza kutekeleza Mtaala uliobereshwa ambao umegawanyika katika mkondo wa Amali na mkondo wa jumla, huku akisisitiza mkondo wa Amali lengo lake ni kujenga Elimu ujuzi kwa mwanafunzi.

Sambamba na ugawaji wa vitabu vya Amali, Dkt. Komba amesema, TET imetoa mafunzo kwa wakuu wa shule wote kuhusu maboresho yaliyofanyika kwenye Mtaala hasa katika mkondo wa Amali, pamoja na namna kutumia Maktaba mtandao ambapo vitabu vyote hupatikana.

Aidha, Dkt Komba amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha zilizosaidia upatikanaji wa vitabu nchini, hasa vitabu vya Amali ambavyo vinagawiwa bure kwa shule zote nchini za Serikali na za binafsi.

Nae, Meneja uchapaji na usambazaji wa vitabu Taasisi ya Elimu Tanzania Bw. Emmanuel Stanslaus ametoa wito kwa walimu kuhakikisha wanatua vitabu hivyo kwa usahihi ili vilete tija kwa wanafunzi kulingana na fani wanazosoma.

Kwa upande wake Mkuu wa shule ya ufundi Nzega na Makamu Mwenyekiti wa wakuu wa shuke Tanzania Bara Mwl. Mwanakombo Juma Martin amesema vitabu hivyo vilivyotolewa bure kwa shule za Serikali na binafsi vitasaidia katika ufundishaji na ujifunzaji kwa wanafunzi hivyo kuleta tija katika utekelezaji wa Mtaala ulioboreshwa mkondo wa Amali.

Nae, Mkuu wa shule ya Ufundi ya wavulana Bwiru iliyopo Mkoani Mwanza Mwl. Thomas Werema amesema Elimu ya Amali inaenda kuwa Mkombozi kwa vijana wa Tanzania, kwani hutoa fursa kwa mw anafunzi kujiajiri, kuajiriwa au kuajiri wengine pindi amalizapo masomo yake, hivyo kusaidia kukabiliana na changamoto ya ajira nchini.












Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Kanali Yahya Ramadhani Kido, Februari 12, 2026 ametembelea Ofisi za Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Kagera kwa lengo la kujitambulisha na kusalimiana na viongozi wa chama ngazi ya mkoa na wilaya.

Ziara hiyo imefanyika siku moja baada ya Kanali Kido kuwasili mkoani Kagera kufuatia uteuzi wake wa hivi karibuni kuwa Mkuu wa Mkoa huo. Katika ziara hiyo, aliambatana na Katibu Tawala wa Mkoa wa Kagera, Bw. Stephen Ndaki, pamoja na Mkuu wa Wilaya ya Bukoba, Mwl. Erasto Sima.

Kanali Kido alipokelewa katika ofisi hizo na Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Mkoa wa Kagera, Ndg. Kareem Amri (MNEC), kwa niaba ya Mwenyekiti wa CCM Mkoa na viongozi wengine wa chama.

Akizungumza wakati wa salamu za utambulisho, Kanali Kido alimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM Taifa, kwa kumuamini na kumteua kushika wadhifa huo.

Ameahidi kutoa ushirikiano wa dhati katika kutekeleza majukumu yake kwa kuzingatia maelekezo na dira ya Mheshimiwa Rais ya kuwahudumia wananchi kwa ufanisi.

Kwa upande wake, Ndg. Kareem Amri alimpongeza Kanali Kido kwa uteuzi huo na kumtakia mafanikio katika majukumu yake mapya. 

Aidha, alimkabidhi Ilani ya CCM inayobainisha ahadi na vipaumbele vilivyokusudiwa kutekelezwa katika Mkoa wa Kagera, akimtaja Mkuu wa Mkoa kuwa msimamizi mkuu wa utekelezaji wa ilani hiyo ngazi ya mkoa.

Ziara hiyo imeelezwa kuwa ni sehemu ya utaratibu wa kuimarisha ushirikiano kati ya Serikali na Chama katika kusimamia na kutekeleza mipango ya maendeleo kwa manufaa ya wananchi wa Kagera.





 

Na Seif Mangwangi, Michuzi TV, Arusha.

Taasisi ya waandishi wa habari ya kusaidia jamii za pembezoni(MAIPAC) imetoa mafunzo kwa waandishi wa habari nchini jinsi ya kuandika habari zinazochochea amani na kulinda usalama wao wakati wa migogoro.

Mafunzo hayo yameshirikisha waandishi wa habari kutoka mikoa ya Dar es Salaam,Mwanza,Geita,Mara,Manyara,Mbeya na Arusha,yalidhaminiwa na shirika la wanahabari la Press Unlimited.

Akifungua mafunzo hayo,Mkurugenzi wa MAIPAC, Mussa Juma aliwataka wanahabari kuandika habari ambazo zinahamasisha amani wakati wa migogoro na kuhakikisha wanakuwa salama.

Juma alisema, habari za upande mmoja ambazo hazizingatii maadili na maslahi mapana ya Umma zimekuwa zikisababisha migogoro katika jamii.

Hata hivyo,aliwataka wanahabari wakati wote wa kazi zao kuzingatia usalama wao,kufanya upembuzi yakinifu wa habari wananayotaka kuandika kabla ya kuandika na baada ya kuandika.

"Tujuwe habari ina madhara gani,inafaida gani ,tusiwe na upande katika hiyo habari na kubwa tuwe tunachukuwa tahadhali za kiusalama wa tunapotumia vyombo vya kidigitari na usalama binafsi"alisema

Wakili  wa kujitegemea John Sendodo akitoa mafunzo kuhusu sheria mbalimbali za masuala ya habari ,aliwataka wanahabari kuzingatia sheria hizo hata kama.zinamapungufu.

"Kuna sheria kadhaa ambazo lazima mzijuwe ikiwepo sheria ya huduma za habari ya mwaka 2016 ,sheria ya makosa ya mitandaoni ya mwaka 2015,kanuni.za maudhui mitandao na nyingine kadhaa tusome tujuwe"alisema

Wakili.Sendodo ambaye anafanyakazi na shirika la.kimataifa la Protection Afrika  akifafanua sheria hizo,vifungu kwa vifungu pamoja na mikataba kadhaa ya kimataifa lnayohusiana na wanahabari aliwataka wanahabari kufanyakazi kwa kutovunja sheria lakini wakitekeleza wajibu wao "alisema.

Mmiliki wa Chuo cha waandishi wa habari cha Fanikiwa kilichopo Arusha,Mwanahabari Joseph Mayagilla akitoa mada katika mafunzo hayo, aliwataka wanahabari wakati wote wa kazi zao kuzingatia maadili ya uandishi.

Mayagilla alisema habari za upande mmoja.zimekuwa na madhara katika jamii na sasa kumeibuka uandishi usiojali maadili ya uandishi.

Hata hivyo, alisema ili kuhakikisha habari.zinakuwa bora ni muhimu kurejesha madawati ya vitengo kadhaa kwenye vyombo vya habari ikiwepo madawati ya habari za uchunguzi,amani na maendeleo,uchumi na mengine kwani yataongozwa na waandishi wabobezi wa eneo husika.

Mtaalam wa masuala ya Saikolojia,Ester Cornelio aliwataka wanahabari wanaokabiliwa na msongo wa mawazo kutojifungia kwenye vyombo vya habari na watoke kupata tiba.

Alisema kunywa pombe kupita kiasi ama kuvuta sana sigara hakuwepo kuondoa Msongo wa mawazo (trouma) bali ni kufika kwa wataalam na kupata tiba ambayo ni ushauri.

Cornelio alisema wanaume wamekuwa wahanga wa msongo wa mawazo ama sonona kwa sababu hawazungumzi ili kutoa yaliyomoyoni tofaufi na wanawake.

Wakichangia mada katika mafunzo hayo, Wanahabari Tausi Mbowe ambaye ni meneja wa dawati ya Kidigitali Star Tv,  na Anthony Mayunga kutoka serengeti media, walieleza umuhimu wa maadili ya uandishi na athari za msongo wa mawazo na mapungufu ya sheria.

Tausi Mbowe alishauri kuendelea kuimarishwa mafunzo ya mara kwa mara kwa wanahabari hasa kuhusiana na sheria na kukabiliana na msongo wa mawazo.

Upande wake mwanahabari Elizabeth Nyivambe kutoka Mbeya na Muta Robet wa Geita na Zakaria Mtigandi wa Manyara walieleza pia umuhimu wa kuendelezwa mafunzo hasa masuala ya matumizi sahihi ya mitandao na usalama kwa wanahabari.







Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni akizungumza wakati wa semina kuhusu Muungano na Mazingira kwa wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iliyofanyika katika Ukumbi wa Pius Msekwa jijini Dodoma, Februari 11, 2026.

*************

Na; Mwandishi Wetu, Dodoma

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni ametoa rai kwa wabunge kupinga na kusahihisha upotoshaji wa taarifa kuhusu Muungano, hususan kupitia mikutano ya hadhara na mitandao ya kijamii.

Ametoa rai hiyo wakati wa semina kuhusu Muungano na Mazingira kwa wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iliyofanyika katika Ukumbi wa Pius Msekwa jijini Dodoma, Februari 11, 2026.

Mhandisi Masauni amesema kuwa Muungano una faida nyingi hivyo ni wakati sasa wabunge kusikiliza na kuwasilisha kwa busara hoja za wananchi kuhusu Muungano

Amesisitiza kuwa wabunge ni nguzo muhimu ya kulinda na kuimarisha Muungano wa Tanzania na wanabeba dhamana ya kihistoria ya kuhakikisha Muungano unaendelea kuwa chanzo cha amani, mshikamano na maendeleo ya Taifa.

Kwa upande wa mazingira, amesema Ofisi ya Makamu wa Rais kwa kushirikiana na wadau imeandaa Programu ya Mageuzi ya Kukijanisha Tanzania ikiwa na lengo la kuleta mageuzi jumuishi na shirikishi yenye matokeo makubwa yanayolenga kuimarisha uhimilivu wa mabadiliko ya tabianchi kwa kuongeza eneo lenye uoto wa kijani kupitia upandaji miti.

Mhe Masauni amesema Julai 17, 2025 Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan alizindua Dira 2050 ambayo imetambua na kuweka nguzo mahususi ya hifadhi na ustahimivu wa mabadiliko ya tabianchi.

“Serikali kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais kwa kushirikiana na wadau imeandaa Programu ya Mageuzi ya Kukijanisha Tanzania ikiwa na lengo la kuleta mageuzi jumuishi na shirikishi yenye matokeo makubwa yanayolenga kuimarisha uhimilivu wa mabadiliko ya tabianchi kwa kuongeza eneo lenye uoto wa kijani kupitia upandaji miti.

“Kwa kuzingatia Dira 2050 imeelekeza Tanzania kuwa kinara barani Afrika katika masuala ya hifadhi na usimamizi wa mazingira, programu ambayo itawasilishwa kwa wabungeitazingatia masuala Uhifadhi wa ardhi oevu, Matumizi ya nishati safi ya kupikia, upandaji miti, biashara ya kaboni, udhibiti wa taka na usafi wa mazingira na udhibiti wa viumbe vamizi,” amesema Mhe. Masauni.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati ya kudumu ya Bunge ya Maji na Mazingira Mhe. Jackson Kiswaga amesema kupitia semina hiyo wamepata uelewa mklubwa kuhusu masuala ya mazingira.

Ameahidi kuwa pamoja na wabunge wenzao wataendelea kuwa mabalozi wazuri kwa wananchi katika kuwafundisha kuhusu uhifadhi wa mazingira endelevu.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni akizungumza wakati wa semina kuhusu Muungano na Mazingira kwa wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iliyofanyika katika Ukumbi wa Pius Msekwa jijini Dodoma, Februari 11, 2026.



Baadhi ya Wabunge wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakiwa katika semina kuhusu masuala ya Muungano na Uhifadhi wa Mazingira iliyotolewa na Ofisi ya Makamu wa Rais, katika Ukumbi wa Pius Msekwa Bungeni Dodoma, Februari 11, 2026.
Mbunge wa Viti Maalumu kundi la Wafanyakazi Mhe. Lucy Mwakyembe kutoka MkoaMjini Unguja akichangia katika semina kuhusu masuala ya Muungano na Uhifadhi wa Mazingira iliyotolewa na Ofisi ya Makamu wa Rais, katika Ukumbi wa Pius Msekwa Bungeni Dodoma, Februari 11, 2026.

PICHA NA OFISI YA MAKAMU WA RAIS
NA EMMANUEL MBATILO, MICHUZI TV

Shirika la Viwango Tanzania (TBS) limeshiriki katika Maonesho ya Biotechnology yaliyofanyika katika Ofisi za Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH), jijini Dar es Salaam, yakilenga kutoa elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa viwango.

Akizungumza katika maonesho hayo, Februari 12, 2026 Jijini Dar es Salaam, Afisa Mdhibiti Ubora wa TBS, Neema Kirway, amesema shirika hilo limeshiriki kikamilifu ili kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu jukumu la TBS katika kudhibiti ubora na usalama wa chakula pamoja na bidhaa nyingine.

Amesema TBS tayari imeanzisha viwango 74 vya Biotechnology, hatua inayolenga kulinda afya, usalama na maslahi ya Mtanzania.

“Kupitia viwango hivi, TBS itahakikisha kuwa bidhaa zote za Biotechnology zinakidhi ubora na usalama kabla ya kumfikia mtumiaji,” amesema Kirway.

Aidha, amebainisha kuwa shirika hilo liko katika mchakato wa kuandaa viwango vingine vya Biotechnology, ambavyo vipo katika hatua za mwisho kabla ya kutangazwa rasmi.

Kirway ametoa rai kwa wadau na wananchi kufahamu kuwa viwango hivyo vinapatikana na vinauzwa katika Makao Makuu ya TBS.

Amesisitiza kuwa TBS itaendelea kusimamia kikamilifu utekelezaji wa viwango ili kuhakikisha bidhaa zote zinazosajiliwa na kupitishwa na shirika hilo ni salama kwa matumizi ya binadamu.

Katika ufafanuzi wake, Kirway amesema teknolojia ya Biotechnology ina mchango mkubwa katika sekta mbalimbali ikiwemo afya, kilimo, viwanda na usalama wa chakula.

“Elimu iliyotolewa katika maonesho haya inasisitiza umuhimu wa wanasayansi kushirikiana, kubadilishana uzoefu na kuimarisha matumizi ya teknolojia na Biotechnology kwa maendeleo ya taifa,” ameongeza.

Kauli mbiu ya maonesho hayo ilikuwa: “Biotechnology Kuimarisha Usalama wa Chakula na Maendeleo ya Jamii na Uchumi.”











Na Munir Shemweta, WANMM ARUSHA

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt. Leonard Akwilapo amewasisitiza wananchi wenye maeneo ya ardhi, kuhakikisha wanayaendeleza kabla serikali haijaanza kuchukua hatua.

Dkt. Akwilapo ametoa kauli hiyo leo tarehe 11 Februari 2026 wakati akifungua Kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) kinachoendelea jijini Arusha.

Akwilapo amesema kumekuwa na tabia kwa baadhi ya wananchi kununua maeneo ya ardhi na kuyahifadhi kwa muda mrefu kama mtaji kwa lengo la kupata faida baadaye.

"Bado natafakari nifanye nini maana sheria ipo, usipoendeleza eneo lako ndani ya miaka mitatu unaweza kunyang'anywa na wengi wanafanya ardhi kama mtaji. Nadhani kuna taasisi maalum za kukuza mitaji, kama vile Soko la Hisa la Dar es Salaa na UTT-AMIS, tumieni hizo taasisi. Huku ardhi tutapishana maneno". Amesema Dkt Akwilapo.

Sheria ya Ardhi Sura Namba 113 kifungu cha 49 inaeleza wazi kuwa mmiliki wa ardhi asiyeendeleza eneo lake katika kipindi cha miaka mitatu serikali inaweza kulichukua eneo lake kutokana na kushindwa kuliendeleza.

Kupitia kikao hicho cha Baraza la wafanyakazi, Mhe. Dkt Akwilapo amewataka waendelezaji milki nchini likiwemo Shirika la Nyumba la Taifa, kuhakikisha wananchi wanapata nyumba bora na za gharama nafuu ili watanzania waweze kuwa na tabasamu.

Amewaasa watumishi wa NHC kuzingatia utu, maadili, uwazi na uaminifu wakati wote wa kutekeleza majukumu yao huku wakiachana na ile dhana ya kuuliza watapata kitu gani ndani ya shirika na badala yake wajiulize watalifanyia nini shirika hilo.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Baraza la wafanyakazi la NHC ambaye pia ndiye Mkurugenzi Mkuu wa Shirika hilo, Bw. Hamad Abdallah amesema shirika lake limekuwa likifanya jitihada mbalimbali za kuhakikisha linaboresha maslahi ya watumishi.

Kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi cha Shirika la Nyumba la Taifa kilichoanza leo tarehe 11 Februari 2026 kinatarajiwa kuhitimishwa Alhamisi tarehe 12 Februari 2026. Kikao hicho pamoja na mambo mengine kinajadili Mizania na Bajeti ya NHC kwa mwaka wa fedha 2026/2027.
Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akizungumza katika Baraza Kuu la Wafanyakazi la Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) wakati wa kikao chake cha siku mbili mkoani Arusha tarehe 11 Februari 2026.



Sehemu ya wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) wakiwa katika kikao tarehe 11 Februari 2026 jijini Arusha
Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) ambaye ni Mkurugenzi wa Shirika hilo Bw. Hamad Abdallah akizungumza katika kikao cha Baraza jijini Arusha tarehe 11 Februari 2026.
Katibu wa TAMICO Taifa Bw, Patenius Rwechungura akizungumza katika kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) jijini Arusha tarehe 11 Februari 2026.
Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo (Katikati) akimkabidhi cheti cha utendaji bora wa kazi Bi. Hindu Nwema, Afisa Uendelezaji wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) wakati wa Kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Shirika hilo tarehe 11 Februari 2026 jijini Arusha. Kushoto ni  Mwenyekiti wa Baraza ambaye ni Mkurugenzi Mkuu wa NHC Bw. Hamad Abdallah
Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akiwa katika picha ya pamoja ya Menejimenti ya Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) pamoja na baadhi ya wajumbe wa Baraza la wafanyakazi wakati wa Kikao kilichofanyika tarehe 11 Februari 2026 jijini Arusha. (PICHA ZOTE NA WIZARA YA ARDHI)

 




Top News