Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali imewasilisha bungeni mapendekezo yatakayowezesha fedha za miradi ya maendeleo katika sekta za maji, barabara na nishati kupelekwa moja kwa moja kwenye mifuko husika ili kuongeza kasi ya utekelezaji wa miradi na kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.

Dkt. Mwigulu amesema hayo leo, Jumamosi Juni 13, 2026, alipokuwa akizungumza na wananchi wa Tarafa ya Ndago katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika Uwanja wa Shule ya Msingi Ndago, Wilaya ya Iramba mkoani Singida.

Amesema hatua hiyo inalenga kuhakikisha fedha zinazotengwa kwa ajili ya utekelezaji wa miradi zinafika moja kwa moja katika sekta husika na kuwezesha utekelezaji wa miradi kufanyika kwa ufanisi na kwa wakati.

“Fedha zote zinazokwenda kwenye barabara, maji na umeme hazitapita tena kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali. Zitakwenda moja kwa moja kwenye mifuko husika ili kuhakikisha utekelezaji wa miradi unaongezeka kasi,” amesema Dkt. Mwigulu.

Waziri Mkuu amesema hatua hiyo itaongeza kasi ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo ambayo utekelezaji wake ulipungua katika kipindi kilichopita kutokana na Serikali kuelekeza rasilimali nyingi katika kukamilisha miradi mikubwa ya kimkakati ya Taifa.

Ametaja baadhi ya miradi hiyo kuwa ni Mradi wa Kufua Umeme wa Julius Nyerere (JNHPP), Daraja la Kigongo–Busisi pamoja na Reli ya Kisasa (SGR), ambayo kwa sasa imekamilika au imefikia hatua kubwa za utekelezaji.

“Tulifanya uamuzi wa kimkakati na wa kizalendo wa kukamilisha miradi hiyo kwa sababu ilikuwa muhimu kwa mustakabali wa Taifa. Sasa miradi hiyo imekamilika au imefikia hatua kubwa za utekelezaji na hivyo kasi ya utekelezaji wa miradi mingine itaongezeka,” amesema.

Katika hatua nyingine, Dkt. Mwigulu amesema Serikali itaongeza kasi ya utekelezaji wa mradi wa Barabara ya Kizaga–Ndago–Sepuka–Singida, ambayo ni miongoni mwa miradi muhimu ya miundombinu inayounganisha maeneo makubwa ya uzalishaji wa mazao katika Wilaya ya Iramba.

Amesema Serikali inatambua umuhimu wa barabara hiyo katika kuchochea shughuli za uzalishaji, biashara na usafirishaji wa mazao hususan katika Tarafa za Ndago na Shelui ambazo ni miongoni mwa maeneo yanayoongoza kwa uzalishaji katika wilaya hiyo.

“Barabara hii ni muhimu sana kwa wananchi wetu. Ni barabara inayounganisha maeneo makubwa ya uzalishaji na ndiyo maana Serikali imeendelea kuipa kipaumbele katika mipango yake ya maendeleo,” amesema.

Aidha, Waziri Mkuu amesema Serikali itaendelea kutekeleza miradi ya madaraja katika maeneo mbalimbali ya Tarafa ya Ndago ili kuondoa changamoto za usafiri na usafirishaji, hususan katika maeneo yanayoathirika wakati wa mvua.

Amesema katika mwaka wa fedha unaoanza Julai 1, 2026, Serikali itaanza utekelezaji wa miradi mbalimbali ya madaraja pamoja na usanifu wa madaraja makubwa yatakayorahisisha mawasiliano na kuimarisha usalama wa wananchi.

Sambamba na hilo, Dkt. Mwigulu amesema Serikali inaendelea na hatua za kuendeleza kilimo cha umwagiliaji katika Bonde la Dengu kupitia usanifu wa miundombinu ya mabwawa na mifumo mingine ya kuhifadhi maji kwa ajili ya kuongeza tija katika uzalishaji wa mazao.

“Usanifu unaendelea katika Bonde la Dengu ili tuweze kuwa na miundombinu ya umwagiliaji itakayowezesha wananchi kuongeza uzalishaji na tija katika kilimo,” amesema.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amesema Serikali imeanza kutafuta suluhisho la kudumu la changamoto zinazowakabili wakulima katika mfumo wa stakabadhi ghalani kwa kuongeza uwekezaji katika ujenzi wa maghala kwenye maeneo ya uzalishaji.

Amesema hatua hiyo itapunguza gharama za usafirishaji wa mazao, kurahisisha uhifadhi wa mazao na kuongeza ufanisi wa utekelezaji wa mfumo wa stakabadhi ghalani.

“Tutajenga maghala katika maeneo ya uzalishaji wa mazao yanayotumia mfumo wa stakabadhi ghalani ili kupata suluhisho la kudumu la changamoto hii,” amesema.

Wakati huo huo, Dkt. Mwigulu ametangaza kupelekwa kwa gari jipya la wagonjwa (ambulance) katika Tarafa ya Ndago ndani ya wiki moja hadi mbili ili kuimarisha huduma za rufaa na dharura kwa wananchi wa eneo hilo.

Amesema ambulance hiyo itasaidia kuhudumia wananchi wa maeneo mbalimbali ya tarafa hiyo na kuongeza ufanisi wa utoaji wa huduma za afya.

“Ndani ya wiki moja hadi mbili ambulance mpya itakuwa imefika Ndago kwa ajili ya kuwahudumia wananchi wa tarafa hii,” amesema.










Na Victor Masangu, Kibaha

Madiwani wa chama cha mapinduzi (CCM) Mkoa wa Pwani wametakiwa kujenga mising imara iya kuwa na uzalendo na Taifa lao ikiwa pamoja na kuweka mikakati kabambe ya kupambana na kero na chanagamoto mbali mbali za wananchi ili kuweza kuzitafuta ufumbuzi.

Hayo yamebainishwa na Mjumbe wa halmashauri kuu ya (CCM) Taifa Mohamed Mchengerwa (MNEC) ambaye pia ni Waziri wa afya wakati wa kufungua mafunzo maalumu kwa madiwani wa CCM Mkoa wa Pwani ambayo yamefanyika katika shule ya uongozi ya Mwalimu Julias Nyerere iliyopo eneo la kwa mfipa katika Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha Mkoa wa Pwani.

Mchengerwa amesema kwamba mafunzo hayo kwa madiwani wa Mkoa wa Pwani watawajengea uwezo mkubwa katika suala zima la kuwatumikia wananchi wao ikiwemo kusikiliza kero na changamotto mbali mbali ambazo zinawakabili wanapaswa kuwa wazalendo.

Kadhalika Mchengerwa amesema kwamba madiwani wanapaswa kuabdilika na kuwa mstari wa mbele katika kwenda kuwa suluhisho katika kuwasikiliza wananchi na kushirikiana nao katika mambo mbali ya kijamii.

"Kwanza kabisa nipende kuchukua fursa hii kumpongeza kwa dhati kabisa Katibu wa chama caha mapinduzi (CCM) kwa kuweza kuwakutanisha kwa mara ya kwanza madiwani wote wa CCM wa Mkoa wa Pwani kwa hivyo kitu kikubwa ninachowaomba ni kuwa wazalendo na nchi yao na kuelekeza nguvu zao katika kutatua kero na changamoto za wananchi,"amebainisha Mchengerwa.

Pia Mchengerwa hakusita kugusia suala la madiwani hao kuwa na upendo, na mshikamano wa pamoja katika maeneo yao kwa lengo la kuweza kushirikiana bega kwa bega na wananchi kwa ajili ya kuweza kuwaletea maendeleo chanya.

Kwa uppande wake Katibu wa chama cha mapinduzi (CCM) Mkoa wa Pwani Ndg. Kiite Mfilinge amesema kwamba lengo kubwa la mafunzo hayo ni kuwakutanisha madiwani hao ili kuwajengea uwezo ikiwa pamoja na kuwakumbushia kutekeleza majukumu yao pamoja na kuwahudumia wananchi.

Katibu huyo amefafanya kwamba katika mafunzo hayo jumla ya madiwani wote wapatao 185 wameweza kupata fursa ya kushiriki na kwamba wamejifunzo mada mbali mbali ikiwemo suala la uzalendo, uwajibikaji, ulinzi na usalama ikiwa pamoja na kuwa na dira ya pamoja katika ngazi ya Mkoa ambayo itaweza kuleta matokeo ya namna bora ya kuwatumikia wannchi.

Kwa upande wake Mwalimu wa shule ya uongozi mwalimu Julias nyerere Profesa Mercellina Chijoriga ambaye pia alikuwa mtoa mada katika mafunzo hayo amesema amebainisha kuwa mafunzo hayo yataweza kuleta tija zaidi ya uwajibikaji katika suala zima la kuwahudumia wananchi katika maeneo yao.

Pia Profesa huyo ametumia mafunzo hayo kuwahimiza madiwani wa Mkoa wa Pwani kuzingatia kwa weledi na ufanisi mkubwa dira ya Taifa ambayo itaweza kuwasaidia kwa kiasi kikubwa kutimiza majukumu yao ipasavyo ikiwemo suala zima la utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Nao baadhi ya madiwani ambao wamehudhuria katika mafunzo hayo akiwemo Ally Simba Diwani wa Kata ya Misusugu pamoja na Diwani wa Kata ya Mwewe omary Msombwe wameahidi kwenda kuyatumia vema mafunzo hayo ambayo wameyapata na kwamba yameweza kuwajengea uwezo mkubwa katika kutekeleza majukumu yao.

Mafunzo hayo ya siku moja yamewajumuisha madiwani wote wa Mkoa wa Pwani waoatao 185 ambapo wamepata fursa ya kujifunz amada mbali mbali ikiwemo suala la uzalendo, ulinzi na amani, uwajibikaji kwa wananchi wao , jinsi ya kusimamia mapato, na kujifunza mambo mbali mbali amabyo yataweza kuwa ni mkombozi mkubwa katika maeneo yao.



MOSHI.

VIJANA wameaswa kutokukubali kurubuniwa, kushawishiwa wala kutumika kwa namna yoyote ili kuhatarisha Amani mshikamano na umoja wa Taifa kwa maslahi binafsi ya watu au makundi yenye nia zisizo njema kwa nchi.

Tamko hilo limetolewa leo na Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi mkoa wa Kilimanjaro, Ivan Moshi mara baada ya kumalizika kwa kikao cha Baraza la UVCCM mkoa wa Kilimanjaro kilichofanyika katika ukumbi wa CCM mkoa.

Akisoma tamko hilo, Moshi alisema kuwa, wanatambua athari kubwa zinazoweza kusababishwa na migogoro, vurugu na mipasuko ya kijamii katika Uchumi na ustawi wa wananchi na kutoa wito kwa vijana kuendelea kuzipuuza kauli, vitendo na propaganda zinazolenga kuleta taharuki, migawanyiko au kuvuruga amani.

“Baraza la UVCCM mkoa wa Kilimanjaro linawapongeza vijana wa Kilimanjaro na Tanzania kwa kuendelea kuonyesha uzalendo, uvumilivu, busara na mshikamano katika kuilinda amani na utulivu wa Taifa letu, tunatambua amani ndio msingi wa maendeleo ya kiuchumi, kijamii na kisiasa” alisema Ivan.





Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimesema kitaendelea kuunga mkono juhudi za Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, za kuharakisha maendeleo ya wananchi huku kikisisitiza kuwa amani, umoja na mshikamano ni msingi muhimu wa maendeleo ya taifa.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma leo, Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa, Itikadi, Uenezi na Mafunzo, Kenani Kihongosi, alisema chama hicho kimeridhishwa na utekelezaji wa miradi ya maendeleo inayofanywa na serikali katika sekta mbalimbali ikiwemo afya, elimu, maji, umeme, barabara, kilimo na uwezeshaji wa wananchi kiuchumi.

Alisema katika ziara za chama zilizofanyika katika mikoa 12 na wilaya 41, viongozi wa CCM wamejionea mafanikio makubwa yaliyopatikana pamoja na kusikiliza changamoto za wananchi ili kuzitafutia ufumbuzi kupitia serikali.

“Tumeshuhudia kazi kubwa inayofanywa na serikali ya CCM chini ya Rais Samia. Fedha nyingi zimepelekwa katika miradi ya maendeleo na wananchi wanaendelea kunufaika na maboresho ya huduma za kijamii katika maeneo mbalimbali nchini,” alisema.

Kihongosi alisema pamoja na mafanikio hayo, baadhi ya changamoto zilizobainika ni migogoro ya ardhi, huduma ya maji katika maeneo machache na vitongoji ambavyo bado havijafikiwa kikamilifu na huduma ya umeme, huku akieleza kuwa serikali inaendelea kuzitatua kupitia bajeti na miradi inayoendelea kutekelezwa.

Alisema maendeleo ya taifa hayawezi kupatikana kwa siku moja bali yanahitaji muda, mipango na uwekezaji endelevu, akibainisha kuwa Tanzania ya sasa imepiga hatua kubwa ikilinganishwa na ilivyokuwa miaka mitano au 10 iliyopita.

Aidha, alimpongeza Rais Samia kwa kuendelea kufungua fursa za kiuchumi kupitia diplomasia ya kimataifa, hatua ambayo imeongeza uwekezaji na ushirikiano wa maendeleo kwa manufaa ya taifa.

Kuhusu Bajeti ya Serikali ya mwaka 2026/27 ya zaidi ya Sh trilioni 62, Kihongosi alisema bajeti hiyo itaongeza kasi ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kuboresha huduma muhimu kwa wananchi, huku akisisitiza kuwa ni ushahidi wa dhamira ya serikali ya kuendelea kuwaletea maendeleo Watanzania.




Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba ameagiza bidhaa zilizochukuliwa kutoka kwa baadhi ya wafanyabiashara wadogo wa Tarafa ya Shelui, Wilaya ya Iramba mkoani Singida kurejeshwa mara moja na kuwataka watendaji wa taasisi za udhibiti kuacha kuchukua mitaji ya wananchi wakati wa utekelezaji wa shughuli za ukaguzi.

Dkt. Mwigulu ametoa maelekezo hayo leo, Jumamosi Juni 13, 2026, alipokuwa akizungumza, kusikiliza na kutatua changamoto za wananchi wa Tarafa ya Shelui katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika Uwanja wa Mnadani, Kata ya Mgongo, Wilaya ya Iramba.

Ametoa agizo hilo baada ya kupokea malalamiko kutoka kwa wafanyabiashara wadogo waliodai kuchukuliwa kwa mafuta yao na baadhi ya watendaji wa taasisi za udhibiti, hali iliyowaathiri katika shughuli zao za kujipatia kipato.

Akizungumza kuhusu suala hilo, Waziri Mkuu alihoji sababu za kuchukuliwa kwa bidhaa hizo na kusisitiza kuwa Serikali haitaki kuona wananchi wanaojitafutia kipato kupitia biashara ndogo ndogo wakinyang’anywa mitaji yao.

“Ulikuwa unafuatilia ziara za Waziri Mkuu? Nilisemaje kuhusu kuchukua bidhaa za wananchi? Kwa nini mmechukua? Huo ni mtaji wake. Dumu moja la mafuta ndiyo mtaji wake. Nimewaambia msikamate hata bakuli la maharage, nyinyi kwa nini mmeenda kuchukua mafuta yao?” amesema Dkt. Mwigulu.

Aidha, aliagiza bidhaa hizo kurejeshwa mara moja kwa wahusika.

“Itarudishwa leo leo. Muwatafute leo leo muwarudishie bidhaa zao. Nimeshaelekeza yarudishwe leo leo na waendelee na shughuli zao,” amesema.

Waziri Mkuu alitumia fursa hiyo kuwataka watendaji wote wanaosimamia shughuli za udhibiti nchini kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia sheria, kanuni na miongozo bila kuathiri shughuli halali za kiuchumi za wananchi.

“Narejea tena, watu wote mnaosimamia mambo ya udhibiti, msichukue bidhaa za wananchi. Hizo ni ofisi zao, hiyo ni mitaji yao. Msichukue bidhaa za wananchi, msichukue bidhaa za Watanzania. Hizo ni ofisi zao,” amesema.

Katika hatua nyingine, Dkt. Mwigulu amesema Serikali itaendelea kuimarisha huduma za maji nchini kupitia utekelezaji wa Mradi wa Maji wa Ziwa Victoria, miradi ya miji 28 pamoja na miradi ya visima kwa lengo la kuongeza upatikanaji wa maji safi na salama kwa wananchi wa Mkoa wa Singida na maeneo mengine nchini.

Amesema miradi hiyo ni sehemu ya jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan za kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora za maji na kupunguza changamoto ya upatikanaji wa huduma hiyo katika maeneo mbalimbali nchini.

“Tunao mradi huu wa kutokea Ziwa Victoria, tunao mradi wa visima, tunao mradi wa miji 28. Miradi yote hii inalenga kuhakikisha wananchi wanapata maji safi na salama. Kabla maji ya Ziwa Victoria hayajafika Dodoma, yatakuwa yameshasambaa katika vijiji mbalimbali vya Wilaya ya Iramba pamoja na maeneo mengine ya Mkoa wa Singida,” amesema.

Waziri Mkuu amesema Serikali itaendelea kufuatilia utekelezaji wa miradi hiyo katika mwaka mpya wa fedha ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya maji kwa uhakika zaidi.

Kuhusu huduma za afya, Dkt. Mwigulu ameagiza kupelekwa kwa gari la wagonjwa (ambulance) katika Tarafa ya Shelui ndani ya wiki mbili ili kuboresha huduma za dharura kwa wananchi wa eneo hilo.

“Ndani ya wiki hizi mbili tutakuwa tumeleta gari la wagonjwa katika Tarafa ya Shelui. Hivi tunavyoongea dereva wa kwenda kulichukua yuko Dar es Salaam. Kwa hiyo ambulance itakuja ili tumalize changamoto hii ambayo wananchi wameiwasilisha,” amesema.

Aidha, amesema Serikali itaendelea kuboresha miundombinu ya afya ikiwemo Kituo cha Afya Mgongo pamoja na kuendeleza mipango ya ujenzi wa miundombinu mingine ya afya katika wilaya hiyo.

Akizungumzia miundombinu ya barabara, Waziri Mkuu amesema Serikali inaendelea na usanifu wa miradi mbalimbali ya barabara na madaraja ili kuboresha mawasiliano na kurahisisha shughuli za kiuchumi na kijamii kwa wananchi wa Wilaya ya Iramba na maeneo jirani.

Wakati huo huo, Dkt. Mwigulu ameagiza viongozi wa Wilaya ya Iramba pamoja na mamlaka husika kukutana na wadau wa sekta ya madini ili kujadili changamoto zilizowasilishwa na wachimbaji wadogo na kutafuta suluhisho litakalolinda maslahi ya wananchi, wawekezaji na Serikali.

“Kesho tukutane tujadili kwa pamoja. Tutawasikiliza wote ili tuweze kupata suluhisho ambalo litalinda maslahi ya wananchi wetu na wakati huo huo kuendeleza uwekezaji,” amesema.






Jumla ya wahatimu 440 waliokuwa wanachama wa club za kodi, kutoka vyuo  vinne vya UDOM, CBE, Mipango na St. John’s, wamefanya mahafali kwenye ukumbi wa Chuo Kikuu cha St. John’s, jijini Dodoma, huku wakitakiwa kutumia elimu waliyoipata kuhamasisha ulipaji wa kodi kwa maendeleo ya Taifa.

Akizungumza katika mahafali hayo Juni 13, 2026, Meneja wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Dodoma, Pendolake Elinisafi, amesema Klabu za Kodi ni jukwaa muhimu la kuwajengea vijana uelewa kuhusu umuhimu wa kodi na mchango wake katika maendeleo ya nchi, amebainisha kuwa vijana wa leo ndio walipakodi wa kesho, hivyo wanapaswa kuandaliwa mapema kuwa raia wenye uelewa wa masuala ya kodi.

Elinisafi amesema Mamlaka ya Mapato Tanzania, ilianzisha Klabu za Kodi mwaka 2018 katika shule za sekondari na vyuo mbalimbali nchini kwa lengo la kuimarisha elimu ya kodi kwa vijana na kujenga kizazi kitakachozingatia ulipaji wa kodi kwa hiari, ameongeza kuwa vijana wana nafasi kubwa ya kuwa mabalozi wa elimu hiyo kwa kuepuka mtazamo hasi dhidi ya kodi na kuanzisha biashara zinazofuata sheria za kodi.

Alieleza kuwa maendeleo mengi yanayoonekana nchini yanatokana na mapato ya ndani yanayokusanywa kupitia kodi, ikiwemo utoaji wa elimu bila malipo, mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu, uboreshaji wa miundombinu, ulipaji wa mishahara ya watumishi wa umma pamoja na utekelezaji wa miradi mikubwa ya kimkakati kama Reli ya Kisasa (SGR), madaraja na huduma nyingine muhimu za kijamii.

Elinisafi aliwataka wasimamizi wa Klabu za Kodi kuendelea kuhamasisha wanafunzi wengi zaidi kujiunga na klabu hizo na viongozi wa klabu kuwaalika maafisa wa TRA katika mijadala mbalimbali ya wanafunzi ili kuendelea kupata elimu sahihi ya kodi, huku akiwatakia wahitimu maisha mema baada ya masomo yao na kuwataka waendelee kuwa mabalozi wazuri wa elimu ya kodi popote watakapokuwa.

Kwa niaba ya wahitimu, viongozi wa Klabu za Kodi wameishukuru TRA kwa mafunzo na elimu waliyoipata, wakisema imewajengea uelewa mkubwa kuhusu umuhimu wa kodi katika maendeleo ya taifa, wakiahidi kuwa mabalozi wazuri  kwa kuhamasisha ulipaji wa kodi kwa hiari.






Uongozi wa Kituo cha Afya Ilazo umefanya kikao cha watumishi wote kwa kipindi cha Januari hadi Juni 2026 kwa lengo la kutathmini utekelezaji wa majukumu, kujadili mafanikio yaliyopatikana, changamoto zilizojitokeza pamoja na kuweka mikakati ya kuboresha utoaji wa huduma za afya kwa wananchi.

Kikao hicho kiliongozwa na Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya Ilazo, Dr. Mathei Kauki na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali pamoja na wageni waalikwa, akiwemo Mwenyekiti wa Kamati ya Uendeshaji wa Kituo, Nkinda Shekilaghe na Afisa Utumishi wa Jiji la Dodoma, Steven Senguo.

Akizungumza katika kikao hicho, Dr. Kauki aliwapongeza watumishi kwa juhudi kubwa wanazoendelea kuzionesha katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora za afya, huku akisisitiza umuhimu wa kuongeza bidii, nidhamu na uwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu ya kila siku.

Kwa upande wake, Afisa Utumishi wa Jiji la Dodoma, Steven Senguo aliwakumbusha watumishi kuendelea kuzingatia maadili ya utumishi wa umma, kufanya kazi kwa weledi, uadilifu na kushirikiana kwa karibu ili kufikia malengo ya taasisi pamoja na kuboresha ustawi wa wananchi.

Aidha, Mwenyekiti wa Kamati ya Uendeshaji wa Kituo hicho, Nkinda Shekilaghe alieleza kuwa ushirikiano kati ya watumishi na viongozi ni msingi muhimu wa mafanikio ya kituo hicho, akihimiza kuendelea kudumisha mshikamano na kujenga mazingira bora ya kazi.

Katika hatua ya kuthamini utendaji kazi, uongozi wa Kituo cha Afya Ilazo ulitoa zawadi na vyeti kwa watumishi pamoja na vitengo vilivyofanya vizuri zaidi katika kipindi hicho. Vitengo vilivyotambuliwa ni pamoja na Kitengo cha Maabara, Kitengo cha RCH (Afya ya Mama na Mtoto) na Kitengo cha Famasi.

Kituo cha Afya Ilazo kinaendelea kutekeleza dhamira yake ya kutoa huduma bora, salama na zenye kuzingatia mahitaji ya jamii.



Na Janeth Raphael MichuziTv


Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) anayeshughulikia Itikadi, Uenezi na Mafunzo, Kenani Kihongosi, amesema chama hicho kimepokea taarifa zinazoonyesha kuwepo kwa baadhi ya makundi yanayodaiwa kupanga njama za kuvuruga amani na utulivu wa nchi.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma leo, Kihongosi amesema CCM imepata taarifa za kuaminika kwamba baadhi ya vyama vya upinzani vinafanya vikao vya siri vinavyolenga kuleta taharuki na kuvuruga hali ya amani iliyopo nchini.

Kutokana na hali hiyo, amewasihi Watanzania kuendelea kuwa walinzi wa amani na kujiepusha na vitendo vyovyote vinavyoweza kuhatarisha usalama, mshikamano na utulivu wa taifa.

“Tunawaomba Watanzania wote kutoshiriki katika mipango au vitendo vyenye nia ya kuvuruga amani ya nchi. Amani ndiyo msingi wa maendeleo yetu, hivyo ni wajibu wa kila mmoja kuilinda na kuitunza,” amesema Kihongosi.

Aidha, amesisitiza kuwa vijana wana nafasi muhimu katika kulinda amani na utulivu wa nchi kutokana na wingi wao na ushawishi mkubwa waliounao katika jamii.

Kihongosi amesema kuna baadhi ya watu ambao wameamua kwenda kinyume na maslahi ya taifa kwa kujiunga na makundi yenye malengo ya kuvuruga amani, akiwataka wananchi kutokubali kushawishiwa na makundi hayo.

Pia amewataka vijana kuwa makini na macho dhidi ya watu au vikundi vinavyoweza kuwatumia kama nyenzo za kutekeleza agenda zinazoweza kuhatarisha usalama wa nchi.

Wakati huo huo, Kihongosi amewataka wananchi kuendelea kumuunga mkono Samia Suluhu Hassan katika juhudi zake za kuimarisha amani, umoja na utulivu wa taifa.

“Amani na utulivu ni nguzo muhimu ya maendeleo ya nchi yetu. Ni jukumu la kila Mtanzania kuhakikisha tunailinda kwa nguvu zote kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho,” amesisitiza.





Na Mwandishi Wetu

UJUMBE wa Tanzania umeunga mkono Mkataba mpya wa Kimataifa unaolenga kulinda haki, usalama na ustawi wa Wafanyakazi wa Mtandaoni ikiwa ni dhamira ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika kuhakikisha maendeleo ya teknolojia na majukwaa ya kidijitali yanakwenda sambamba na ulinzi wa utu wa mfanyakazi, usawa na haki za msingi za kazi.

Hayo yamejiri wakati wa hafla ya kuhitimisha Mkutano Mkuu wa 114 wa Shirika la Kazi Duniani (ILO) leo tarehe 12 Juni, 2026 uliyofanyika katika Ukumbi wa Umoja wa Mataifa, Jijini Geneva, Uswisi ambapo kupitia Mkutano huo, taarifa za Kamati mbalimbali zilipokelewa ikiwemo Kamati ya Upangaji wa Viwango vya Kazi ambayo imewezesha kuandaliwa na kupitishwa kwa Mkataba wa Kazi kuhusu Wafanyakazi Mtandaoni wa Mwaka 2026.

Katika kupitisha Mkataba huu, kura 406 zimeunga mkono kupitishwa kwa Mkataba husika, nchi Nane (8) hazijaunga mkono kupitishwa Mkataba na nchi 36 hazijaonesha kuwa upande wowote.

Mkataba huo mpya umeweka misingi ya kimataifa kuhusu: Ulinzi wa haki za msingi za wafanyakazi wa mtandaoni; Uainishaji sahihi wa hadhi ya ajira kulingana na hali halisi ya kazi; Malipo ya haki na uwazi; Upatikanaji wa hifadhi ya jamii; Uwazi na udhibiti wa mifumo ya kidijitali ikiwemo haki ya maelezo na mapitio ya maamuzi yanayofanyika kidijitali pamja na Ulinzi wa taarifa binafsi na haki ya kupata kusuluhisha migogoro.

Akitoa hotuba yake wakati wa kufunga Mkutano huo, Rais wa Mkutano Mkuu wa 114 wa ILO, Juan Castillo, amesisitiza kuhusu mafanikio makubwa yaliyopatikana kupitia makubaliano ya kihistoria kuhusu kazi za staha kwa kazi zinazofanyika kidijitali.

Amesema, kutokana na ukuaji wa sayansi na teknolojia, kumekuwa na ongezeko kubwa la matumizi ya Akili Unde (AI), hivyo, amesisitiza kwamba teknolojia inapaswa kutumika ili kuendeleza ustawi wa binadamu na si kuondoa utu wa wafanyakazi au kuongeza ukosefu wa usawa, huku akihimiza matumizi ya Akili Unde yanayozingatia maadili na haki za kazi.

Kwa upande mwengine, Juan Castillo amepongeza mfumo wa Utatu wa Shirika la Kazi Duniani (ILO) umekuwa ni chombo muhimu cha kuwaleta pamoja waadau husika, yaani Serikali, Waajiri na Wafanyakazi, akieleza kuwa majadiliano na mafikiano yaliyofikiwa katika siku 12 za Mkutano huo yamethibitisha umuhimu wa mazungumzo ya kijamii katika kukuza ustawi wa Sekta ya Kazi.

Upitishwaji wa Mkataba wa Kazi Kuhusu Wafanyakazi wa Mtandaoni haumaanishi kuanza kwa utekelezaji wa baadhi ya masuala yaliyoanishwa katika Mkataba huo kwa kuwa Serikali ya Awamu ya Sita kupita Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano pamoja na Wadau wengine wa masuala ya Kazi,

Ulianzishwa kutekeleza viwango vilivyotajwa katika Mkataba huo ambapo miongoni mwa jitihada zilizochukuliwa ni pamoja na: Kukuza na kutambua wafanyakazi wa mitandaoni kwa kuimarisha uchumi wa kidijitali; Kuimarisha ulinzi wa matumizi ya mtandao kupitia Sheria na miongozo kama vile Sheria ya Makosa ya Mtandaoni na Kanuni za Ulinzi wa Taarifa Binafsi.

Aidha, utoaji wa mafunzo ya TEHAMA kwa vijana yanalenga kuongeza fursa za ajira za kidijitali na kuwasaidia wafanyakazi wa mitandaoni kufanya kazi kwa ufanisi zaidi na kuingia kwenye soko la kimataifa na uimarishaji wa mifumo ya kidijitali umeendelea kupanua miundombinu ya TEHAMA kama vile upanuzi wa mtandao wa Vijijini na Mijini ili kuwezesha watu wengi zaidi kufanya kazi mtandaoni kwa ufanisi.

Mkutano Mkuu wa 114 wa Shirika la Kazi Duniani (ILO) umihitimishwa leo na kukamilika kwake ni mwanzo wa Kikao cha 357 cha Bodi ya Magavana ya ILO unaofanyika tarehe 12 na 13 Juni, 2026 Geneva, Uswisi ambapo Tanzania pia ni Mjumbe wa Bodi hiyo ikiwakilisha nchi za Ukanda wa Afrika Mashariki.














Na Said Mwishehe,Michuzi TV

MSANII maarufu nchini katika muziki wa kizazi kipya a.k.a Bongo Fleva Rashidi Makwiro maarufu Chid Benz ametoa ya moyoni kwa kuishukuru Mamlaka ya Kudhihiti na Kupambana na Dawa za Kulevya na wote waliomuwezesha kuachana na matumizi ya dawa za kulevya.

Chid Benz ametoa shukrani hizo Juni 12,2026 jijini Dar es Salaam wakati wa uzinduzi wa filamu iliyopewa jina Kifurushi ambayo ni maalum kuelezea madhara ya dawa za kulevya.

Pia ni filamu inayotoa elimu kwa madereva,makondakta na abiria kuwa makini kwa kutosafirisha vifurushi ambavyo hawajui ndani yake kuna nini.Ni filamu iliyoandaliwa na mamlaka hiyo kwa kushirikiana na Bodi ya Filamu Tanzania pamoja na LATRA.

Katika uzinduzi wa filamu hiyo msanii Chid Benz ambaye ubora wake katika muziki umeeendelea kubaki katika viwango vya daraja la juu aliyepewa jukum la kutoa burudani kupitia vibao vyake kadhaa kikiwemo Dar es Salaam Stand up alitumia nafasi hiyo kutoa shukrani zake kwani kwa sasa ameachana kabisa na dawa za kulevya .

“Kamishina wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya Aretas Lyimo nakushukuru sana.Uliamua kunisaidia kuniondoa kwenye matumizi ya dawa za kulevya.Nakushukuru kwasababu pia nikikupigia simu unapokea,meseji unajibu.”

Akiendelea kuzungumza Chidi Benzi amesema “natamani niwaambie ndugu zangu tuache dawa za kulevya lakini sidhani kama sasa hivi watu wanatumia maana nahisi dawa hizo hazipo mtaani.Kuna saa zingine naongea na ndugu zangu nauliza vipi mtaani freshi wanaambia sio freshi.

“Kwahiyo hiyo kazi ambayo imefanyika ya kukomesha dawa za kulevya imefanyika kwa ukubwa kwani zamani ilikuwa kwa mfano nikikaa kama hapa nikiuliza eh bwana vipi hapa naambiwa freshi pita nyuma lakini sasa nakwambia ah sio freshi Chidi.”

Ameongeza kwa upande yeye ameacha kabisa kutumia dawa za kulevya na sasa hivi hata bila kumwambia mtu kama anatumia mtu mwenyewe anamuwahi kumwambia ameacha.

“Hivyo nashukuru Serikali, nashukuru Mamlaka ,nakushukuru kila mtu nashukuru na

leo tuko pamoja na kuonyesha kwamba nina nguvu za kutosha ninaburudisha,”amesema na kusisitiza naye anaungana na Mamlaka kuwahimiza wamiliki wa mabasi,madereva,makondakta na wananchi kwa ujumla kushiriki kikamilifu katika kutoa taarifa.

Aidha amesema filamu hiyo iliyozinduliwa itasaidia kuongeza uelewa wa jamii na kuimarisha mapambano dhidi ya usafirishaji wa dawa za kulevya nchini.








Top News