SHIRIKA la Viwango Tanzania (TBS) Kanda ya Magharibi imefanikiwa kutoa leseni 129 kwa wazalishaji wa bidhaa katika kanda hiyo, huku leseni 99 kati ya hizo zikitolewa kwa wajasiriamali wadogo.

Akizungumza na waandishi wa habari kuhusu mafanikio ya TBS katika sekta ya viwanda, Meneja wa TBS wa Kanda hiyo, Bw. Hamisi Seleleko amesema hatua hiyo inaonesha jitihada za shirika hilo katika kuwasaidia wazalishaji kufuata viwango vinavyotakiwa na hivyo kuimarisha ubora wa bidhaa zinazozalishwa nchini.

Amesema mafanikio hayo pia yametokana na mahusiano mazuri kati ya TBS na Tawala za Mikoa, Wilaya pamoja na Halmashauri katika kanda hiyo, hali iliyosaidia kuimarisha ukaguzi na utekelezaji wa sheria.

Kutokana na ushirikiano huo, wananchi wamekuwa wakipatiwa elimu ya viwango mara kwa mara jambo ambalo limechangia kupungua kwa bidhaa hafifu sokoni, hususan za chakula na vipodozi.

Bw. Seleleko amesema kiasi cha bidhaa hafifu kilichokamatwa kimepungua kutoka tani 11 mwaka 2024 hadi kufikia tani 8 mwaka 2025.

Aidha, amesema TBS Kanda ya Magharibi imefanikiwa kusajili majengo zaidi ya 2,100 ya chakula na vipodozi, ikilinganishwa na mwaka 2020 wakati ofisi hiyo ilipofunguliwa ambapo majengo 400 pekee ndiyo yaliyokuwa yamesajiliwa.

Amesema hatua hiyo inaonesha kuongezeka kwa uelewa wa wazalishaji na wafanyabiashara kuhusu umuhimu wa kuzingatia viwango katika uzalishaji wa bidhaa ili kulinda afya na usalama wa watumiaji.
  


Tume ya Ushindani (FCC) imesema wazalishaji wa vifaa vya ujenzi wana wajibu wa kumlinda mlaji kwa kuhakikisha wanazalisha na kuuza bidhaa zenye ubora unaolingana na thamani ya fedha anayolipa mnunuzi.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa semina kwa wazalishaji wa vifaa vya ujenzi kuelekea kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Mlaji Duniani yenye kauli mbiu isemayo "Bidhaa Salama, Imani kwa Mlaji", Mkurugenzi wa Udhibiti wa Mienendo ya Bidhaa Inayokatazwa na Sheria ya Ushindani wa FCC, Bi. Magdalena Utouh, kwa niaba ya Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, amesema ulinzi wa mlaji ni miongoni mwa majukumu makuu ya Tume hiyo.

FCC imeeleza kuwa suala la usalama wa bidhaa za ujenzi si suala la biashara pekee, bali ni suala la usalama wa jamii na maendeleo ya Taifa kwa ujumla hivyo ni muhimu kwa wazalishaji kuzingatia viwango vinavyotakiwa katika uzalishaji wa vifaa vya ujenzi ili kuepusha uwepo wa bidhaa zisizo na ubora sokoni, ambazo zinaweza kusababisha hasara kwa watumiaji na kudhoofisha imani ya wananchi katika bidhaa hizo.

Amesema FCC itaendelea kufuatilia mwenendo wa soko la bidhaa za ujenzi ili kuhakikisha haki za walaji zinalindwa na wananchi wanapata bidhaa salama na zenye ubora unaokidhi viwango vinavyotakiwa.
Bi. Utouh amewataka wazalishaji wa vifaa vya ujenzi kuendesha biashara zao kwa kuzingatia sheria na kanuni za ushindani wa haki, hatua ambayo itasaidia kujenga soko lenye ushindani wa kweli unaolinda maslahi ya walaji pamoja na kuchochea maendeleo ya sekta ya ujenzi nchini.

Ameeleza kuwa sekta ya ujenzi ni mhimili muhimu wa ukuaji wa uchumi wa taifa, hivyo uzalishaji wa vifaa vya ujenzi unapaswa kufanyika kwa kuzingatia viwango stahiki na thamani halisi ya fedha inayolipwa na mlaji.

“FCC ina jukumu la kufuatilia mwenendo wa ushindani katika soko ili kuhakikisha hakuna makubaliano ya kupanga bei miongoni mwa wafanyabiashara ambayo yanaweza kumuathiri mlaji,” amesema Bi.Magdalena
 
Amesema Tume haitavumilia vitendo vyovyote vinavyomuumiza mlaji, akisisitiza kuwa sheria na miongozo ya ushindani ipo wazi na wazalishaji wanapaswa kuizingatia kikamilifu.

Hata hivyo amesema mikutano na majadiliano kati ya FCC na wadau wa sekta ya ujenzi itaendelea kufanyika mara kwa mara ili kuimarisha ushindani wa soko na kuhakikisha walaji wanapata bidhaa na huduma bora.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Huduma za Wanachama wa Shirikisho la Wamiliki wa Viwanda Tanzania (CTI), Bi. Neema Mhondo, amesema sekta ya ujenzi ina mchango mkubwa katika kukuza uchumi wa nchi pamoja na kutoa ajira kwa wananchi.

Hata hivyo, amesema wazalishaji wa ndani wanakabiliwa na changamoto ya uwepo wa bidhaa bandia sokoni, hali inayofanya viwanda vya ndani kupata ugumu katika ushindani kutokana na gharama kubwa za uzalishaji na uendeshaji wa biashara.

Semina hiyo ya siku moja imefanyika Machi 11, 2026 katika Ukumbi wa Mikutano wa Ngorongoro katika Ofisi za FCC, Jijini Dar es Salaam. 
Mkurugenzi wa Udhibiti wa Mienendo ya Bidhaa inayokatazwa na Sheria ya Ushindani wa FCC Bi.Magdalena Utouh akizungumza wakati akifungua Semina ya Wadau wa Uzalishaji wa Vifaa vya Ujenzi ,jijini Dar es Salaam.
















 

Morogoro, Tanzania, 10 March 2026: Miaka ya hivi karibuni, magonjwa yasiyoambukiza yanaendelea kuwa changamoto kubwa kwa afya ya jamii nchini Tanzania. Magonjwa kama shinikizo la damu, kisukari, magonjwa ya moyo pamoja na saratani yanaongezeka kwa kasi, huku wengi wakigundulika wakiwa tayari katika hatua za mwisho za ugonjwa kutokana na kukosekana kwa uchunguzi wa mapema na uelewa mdogo kuhusu kinga na dalili zake.

Kwa mujibu wa takwimu za afya nchini, magonjwa yasiyoambukiza yanachangia takribani asilimia 34 ya vifo vyote nchini Tanzania, jambo linaloonyesha umuhimu wa kuimarisha juhudi za kinga, uchunguzi wa mapema pamoja na elimu kwa jamii kuhusu namna ya kujikinga na magonjwa hayo.

Kwa jamii nyingi, hasa zile zilizo mbali na huduma za afya au zenye changamoto za kifedha, watu wengi huchelewa kufanya uchunguzi wa afya hadi pale hali inapokuwa mbaya zaidi. Hali hii huongeza hatari za kiafya ambazo zingeweza kuzuilika kupitia uchunguzi wa mapema na ushauri wa kitaalamu.

Kwa kutambua umuhimu wa kukabiliana na changamoto hii, sekta binafsi zimeendelea kushirikiana na serikali katika kuboresha upatikanaji wa huduma za afya kwa jamii. Katika kuunga mkono juhudi hizi, Vodacom Foundation Tanzania imeanza zoezi la Kambi ya Matibabu ya Bure kwa ajili ya uchunguzi wa magonjwa yasiyoambukiza kwa wakazi wa Morogoro, ikilenga kuwasogezea wananchi huduma muhimu za uchunguzi, ushauri na elimu ya afya.

Baada ya kufanikisha kambi ya afya ya bure iliyofanyika hivi karibuni Zanzibar iliyohudhuriwa na zaidi ya wananchi 2000 waliopata huduma mbali mbali za uchunguzi wa afya na ushauri wa kitabibu, sasa mpango huo unaelekea Morogoro ili kuwafikia wananchi wengi zaidi.

Kwa kushirikiana na madaktari bingwa kutoka Muhimbili National Hospital, Vodacom Tanzania Foundation inaleta tena huduma za uchunguzi na matibabu bila malipo ili kusogeza huduma muhimu za afya karibu zaidi na wananchi.

Kambi hiyo ya afya itafanyika katika Viwanja vya Shule ya Kilosa Mjini mkoani Morogoro, kuanzia tarehe 10 hadi 13 Machi 2026, ambapo wananchi watapata huduma mbalimbali za uchunguzi ikiwemo shinikizo la damu, kisukari, magonjwa ya moyo pamoja na ushauri wa kitaalamu kuhusu namna ya kujikinga na kudhibiti magonjwa yasiyoambukiza.

Mpango huu ni sehemu ya juhudi za muda mrefu za Vodacom Tanzania Foundation katika kusaidia jamii kupitia huduma za afya, elimu na miradi mingine ya maendeleo, huku ukilenga kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu umuhimu wa uchunguzi wa mapema na kinga dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza.

Akizungumza Katika hafla hiyo, Mkuu wa Wilaya ya Kilosa, Shaka Hamdu Shaka, alipongeza Vodacom Tanzania Foundation pamoja na Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa kuandaa makambi haya ya afya yanayotoa huduma bure kwa wananchi wa Kilosa.

“Tunapenda kuishukuru Vodacom Tanzania Foundation na Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa kuwa mdau muhimu katika sekta ya afya na kwa kuendelea kuleta huduma hizi karibu zaidi na wananchi. Kambi hii ya huduma za afya imeandaliwa kwa kuzingatia jiografia ya eneo hili pamoja na mahitaji halisi ya wananchi’

Akielezea kuhusu mpango huo, Meneja wa Vodacom Tanzania Foundation, Sandra Oswald, alisema kuwa afya bora ya jamii ni msingi muhimu wa maendeleo ya taifa.

“Afya njema ndiyo msingi wa jamii yenye nguvu na tija. Kupitia kambi hizi za matibabu bure tunalenga kuwahamasisha wananchi kuchukua hatua za mapema kuhusu afya zao kwa kufanya uchunguzi, kupata ushauri wa kitaalamu na kujifunza njia bora za kujikinga na magonjwa yasiyoambukiza,” alisema.

Aliongeza kuwa Vodacom Tanzania Foundation itaendelea kushirikiana na wataalamu wa afya pamoja na wadau mbalimbali kuhakikisha huduma za kinga na uchunguzi wa magonjwa yasiyoambukiza zinawafikia wananchi wengi zaidi, hususan wale wanaokabiliwa na changamoto za kifedha au umbali wa huduma za afya.

Mpango huu pia unaendana na malengo ya maendeleo endelevu ya kimataifa, hususan Sustainable Development Goal 3 yanayolenga kuhakikisha afya bora na ustawi kwa wote.

Vodacom Tanzania Foundation inawahimiza wakazi wa Morogoro kujitokeza kwa wingi katika kambi hiyo ili kufanyiwa uchunguzi wa afya na kupata elimu kuhusu namna ya kujikinga na magonjwa yasiyoambukiza, kwani uchunguzi wa mapema na uelewa sahihi ni hatua muhimu katika kujenga jamii yenye afya bora na mustakabali imara.







Balozi wa Tanzania nchini Zimbabwe, Kamishna wa Polisi (CP) Suzan Kaganda, amekutana na kufanya mazungumzo na Mkurugenzi wa Idara ya Afrika na Asia katika Wizara ya Mambo ya Nje na Biashara za Kimataifa ya Zimbabwe, Bw. Mqabuko Dube.

Katika mazungumzo hayo yaliyofanyika nchini Zimbabwe, viongozi hao walijadili masuala mbalimbali ya ushirikiano kati ya Tanzania na Zimbabwe, hususan katika kuimarisha mahusiano ya kidiplomasia na ushirikiano wa kikanda.

Aidha, pande zote mbili zilikubaliana kuendeleza na kuimarisha ushirikiano uliopo kati ya nchi hizo mbili, pamoja na kushirikiana kwa karibu katika utekelezaji wa majukumu yao kwa lengo la kuchochea maendeleo ya pamoja na kuimarisha uhusiano wa kirafiki uliopo kati ya Tanzania na Zimbabwe.

Na Mwandishi Wetu, Arusha.

Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela kwa kushirikiana na Taasisi ya Global Education Link Ltd wamesaini hati ya makubaliano ya ushirikiano yenye lengo la kukuza tafiti, ubunifu na maendeleo ya kisayansi.

Makubaliano hayo yatakayosaidia kuandaa kizazi kipya kitakacholeta mapinduzi ya kiuchumi na kiteknolojia Barani Afrika na duniani kwa ujumla.

Ushirikiano huo unatarajiwa kufungua milango ya fursa mpya katika sekta ya elimu, utafiti na ubunifu, pamoja na kuitangaza taasisi hiyo kimataifa ili dunia itambue kuwa Tanzania ina taasisi inayozalisha vipaji na teknolojia za kisasa kupitia ushirikiano na vyuo vikuu mbalimbali vya nje ya nchi.

Akizungumza mara baada ya kusainiwa kwa makubaliano hayo, Makamu Mkuu wa Taasisi ya Nelson Mandela, Profesa Maulilio Kipanyula, alisema Afrika ina hazina kubwa ya vipaji ambavyo vikisimamiwa na kupangwa vizuri vinaweza kutoa suluhisho la changamoto mbalimbali zinazoikabili jamii.

Profesa Kipanyula alisisitiza kuwa ubunifu na maendeleo ya kisayansi hayawezi kufikiwa bila ushirikiano wa taasisi mbalimbali, akibainisha kuwa makubaliano hayo ni hatua muhimu katika kuongeza idadi ya wanafunzi, hususan wanafunzi wa kimataifa, pamoja na kuchangia kukuza uchumi.

Alisema makubaliano hayo ni ya kimkakati katika kuhakikisha elimu inayotolewa inaendelea kuimarika kimataifa kwa kuvutia vipaji vya vijana kusoma na kuwasilisha bunifu zao kupitia Taasisi ya Nelson Mandela.

Aidha, alieleza kuwa anatamani kuona taasisi hiyo ikiendelea kuzalisha na kulea vipaji vya vijana pamoja na ubunifu mbalimbali utakaosaidia kuchochea maendeleo katika majukwaa ya kitaifa na kimataifa.

“Tunataka tafiti zetu na matokeo yake yawafikie wananchi kwa haraka zaidi, ambapo ubunifu na maarifa vitakuwa na mchango mkubwa kwa jamii. Utafiti na ubunifu lazima viwe na uwezo wa kutatua changamoto za watu,” alisema Profesa Kipanyula.

Naye Mkurugenzi wa Taasisi ya Global Education Link Ltd, Abdullmalik Mollel, alisema ushirikiano huo umejikita katika kuimarisha masuala ya kitaaluma, uwekezaji na matumizi ya teknolojia ili kuongeza tija katika sekta ya elimu na uchumi.

Alisema elimu inayotolewa kwa wanafunzi inapaswa kuwa na mchango wa moja kwa moja katika kukuza uchumi na maendeleo kwa kutumia teknolojia, maarifa na mitaji.

“Elimu anayopewa mwanafunzi inapaswa kusaidia kukuza uchumi na kuleta maendeleo kupitia teknolojia, maarifa na uwekezaji. Ushirikiano wa maarifa kati ya vyuo vikuu mbalimbali utaongeza tija katika kukuza uchumi unaotegemea teknolojia,” alisema Mollel.

Aliongeza kuwa makubaliano hayo ni mwanzo wa safari ya ushirikiano wa muda mrefu kati ya taasisi hizo mbili, wenye lengo la kuimarisha ushirikiano wa vyuo vikuu na kuleta mabadiliko chanya katika sekta ya elimu, utafiti na maendeleo ya jamii kwa ujumla.








Shirika lisilo la kiserikali la Kikristo ECHO East Africa kutoka Ngaramtoni jijini Arusha limefanya warsha ya mafunzo kwa vitendo kwa waandishi wa habari kutoka vyombo mbalimbali vya habari jijini Arusha kuhusu Kilimo Ikolojia (Agroecology).

Shirika hilo linafanya kazi katika nchi za Afrika Mashariki pamoja na baadhi ya nchi za Kusini mwa Afrika, Lengo ni kuwasaidia wakulima, hususan wakulima wadogo, kwa kuwapatia mbinu mbadala, elimu, ujuzi na maarifa ili kuongeza uzalishaji wa mazao yao kwa kutumia mbinu rafiki kwa mazingira, ikiwemo kilimo ikolojia.

Warsha hiyo ya mafunzo kwa vitendo imefanyika kwa siku mbili na Dhumuni la mafunzo hayo ni kuwaleta pamoja waandishi wa habari kutoka vyombo mbalimbali ili kuwafahamisha juu ya uwepo wa shirika hilo, kuelewa shughuli mbalimbali zinazotekelezwa, pamoja na kuwapa elimu kuhusu kilimo ikolojia.

Katika mafunzo hayo, waandishi wa habari wamepata fursa ya kufanya ziara katika maeneo mbalimbali ndani ya shirika hilo na kujifunza masuala kadhaa ya kilimo ikolojia. Miongoni mwa mambo waliyojifunza ni pamoja na mbinu za uvunaji wa maji ili kupunguza mmomonyoko wa udongo, kilimo mseto, upandaji wa miti, na matumizi ya mazao yanayofunika ardhi ili kulinda rutuba ya udongo.

Aidha, washiriki wametembelea miradi mbalimbali inayotekelezwa na shirika hilo, ikiwemo benki ya mbegu, uzalishaji wa biogas, matumizi ya mitambo ya kukaushia vyakula, pamoja na kutembelea wakulima ambao ni wanufaika wa mbinu za kilimo ikolojia.

Kilimo Ikolojia (Agroecology) ni mfumo wa kilimo unaochanganya kanuni za ikolojia, yaani mazingira ya asili, na uzalishaji wa mazao. Lengo lake ni kuzalisha chakula kwa njia rafiki kwa mazingira, endelevu na yenye kunufaisha wakulima pamoja na jamii kwa muda mrefu.

Wataalamu wa kilimo wanaendelea kuhamasisha matumizi ya kilimo ikolojia kama njia mbadala ya kuongeza uzalishaji wa chakula huku wakilinda mazingira. Mbinu hii inahusisha matumizi ya rasilimali za asili, kupanda mazao mchanganyiko, pamoja na kupunguza utegemezi wa kemikali shambani.







-Vodacom Tanzania Foundation Imejenga matundu 10 ya vyoo Shule ya Msingi Mkata

Vodacom Tanzania Foundation kwa kushirikiana na Twende Butiama pamoja na Stanbic Bank wamejenga matundu 10 ya kisasa ya vyoo katika Shule ya Msingi Mkata iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Handeni mkoani Tanga, ikiwa ni sehemu ya kurudisha kwa jamii.

Akipokea matundu hayo 10 ya vyoo kutoka kwa Meneja Mauzo Mwandamizi wa Vodacom Tanzania Kanda ya Kaskazini, Andrew Temu, kwa niaba ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Handeni, Yibarila Chiza alisema vyoo hivyo vitasaidia kulinda afya za wanafunzi pamoja na kuwafanya kuwa mabalozi wa kuhamasisha matumizi ya vyoo bora na vya kisasa majumbani mwao.

Aidha alisema kuwa vyoo hivyo vitachochea ufaulu wa wanafunzi kwa kupunguza changamoto ya uhaba wa matundu ya vyoo katika shule hiyo, na hivyo kuwawezesha wanafunzi kupata mazingira bora ya kujifunzia. Alitoa shukrani kwa wadau hao kwa msaada huo walioutoa kwa shule hiyo.

Kwa upande wake, Meneja Mauzo Mwandamizi wa Vodacom Tanzania Kanda ya Kaskazini, Andrew Temu, alisema Vodacom Tanzania Foundation inaangazia maeneo matatu makuu ambayo ni afya, mazingira na elimu.

Alisema ili mwanafunzi aweze kusoma vizuri anahitaji kuwa katika mazingira rafiki yasiyokuwa na msongo wa mawazo, hivyo ujenzi wa vyoo hivyo utasaidia wanafunzi hasa wenye mahitaji maalum na kuwapa muda zaidi wa kukaa darasani badala ya kupoteza muda kusubiri foleni ya huduma ya choo.

Naye Mwenyekiti wa msafara wa Twende Butiama, Gabriel Landa, alisema wao kama Twende Butiama wameamua kutumia baiskeli kama njia ya kumuenzi Baba wa Taifa kwa kuhamasisha wananchi kuboresha sekta za afya, elimu na mazingira kupitia programu mbalimbali za uhamasishaji.

Awali akitoa taarifa ya shule, Mwalimu Mkuu Msaidizi wa Shule ya Msingi Mkata, Daliana Majatta, alisema matundu hayo ya vyoo yamesaidia kupunguza uhitaji wa vyoo katika shule hiyo, ingawa bado wanahitaji jumla ya matundu 28 ili kukidhi mahitaji yaliyopo.

"Pamoja na mafanikio hayo, shule yetu bado ina changamoto mbalimbali zinazoifanya isiwe ya kisasa zaidi, ikiwemo miundombinu ya madarasa kwa ajili ya wanafunzi wenye mahitaji maalum pamoja na upungufu wa madawati 300, wakati idadi ya wanafunzi ni 2,023," alisema Majatta.

Mbali na ujenzi wa matundu hayo 10 ya vyoo, Vodacom Tanzania Foundation pia imewahi kutoa misaada mbalimbali katika shule hiyo ikiwemo viti mwendo kwa wanafunzi wenye mahitaji maalum, magodoro, vitanda pamoja na mashuka.
Meneja Mauzo Mwandamizi wa Vodacom Tanzania Kanda ya Kaskazini, Andrew Temu, akizungumza wakati wa makabidhiano ya matundu 10 ya vyoo vya kisasa vilivyojengwa na Vodacom Tanzania Foundation katika Shule ya Msingi Mkata iliyopo wilayani Handeni mkoani Tanga. Ujenzi wa vyoo hivyo unalenga kutimiza dhamira ya Vodacom ya kuchangia kuboresha mazingira ya kujifunzia kwa wanafunzi wote, huku ikiangazia afya na ustawi wa wanafunzi kupitia miradi ya maendeleo ya jamii. Tukio hilo lililofanyika jana lilihudhuriwa na Yibarila chiza, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji Wilaya ya Handeni (kulia), Meneja Uhusiano wa masuala ya serikali wa Vodacom Tanzania Grace Lyon (Kushoto), Mwenyekiti wa Msafara wa Twende Butiama Gabriel Landa (Wa pili kushoto) pamoja na wazazi, walimu na wanafunzi wa shule hiyo.
Uongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Handeni, Timu ya Vodacom, Wawakilishi wa Twende Butiama na Walimu wakiwa kwenye picha ya pamoja baada ya kufunguliwa kwa vyoo vipya vya kisasa vilivyotolewa na Kampuni ya Mawasiliano na teknolojia ya Vodacom Tanzania Plc katika Shule ya Msingi Mkata, iliyoko wilaya ya Handeni mkoani Tanga.

Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Handeni, Bw Yibarila Chiza na Meneja Mauzo Mwandamizi wa Vodacom Tanzania Plc Kanda ya Kaskazini, Andrew Temu wakikata utepe ikiwa ni ishara ya kufungua rasmi vyoo vya kisasa 10 vilivyojengwa na Kampuni hiyo katika shule ya Msingi Mkata wilayani Handeni mkoani Tanga, Vodacom imetimiza ahadi iliyotolewa kwa shule hiyo wakati wa msafara wa waendesha baiskeli wa 'Twende Butiama' uliopita shuleni hapo mwaka jana ikiwa ni ishara ya kumuenzi Baba wa Taifa Mwl JK Nyerere. Tukio Hilo lilifanyika jumatatu wiki hii mjini Mkata.

Baadhi ya Wanafunzi wa Shule ya Msingi Mkata iliyopo wilayani Handeni Mkoani Tanga, wakifurahia uwepo wa vyoo vipya na vya kisasa 10, vilivyotolewa na Kampuni ya Mawasiliano na Teknolojia ya Vodacom Tanzania. Vyoo hivi vinalenga kuboresha mazingira ya kujisomea ya wanafunzi hao.

Na: Dkt. Reubeni Lumbagala, Tanga

Watoto wana haki zao za msingi. Wanapaswa kupendwa, kulindwa, kusikiliza, kupewa malezi na matunzo. Pia, watoto wanapaswa kupewa mahitaji yote ya msingi yaani chakula, mavazi na malazi. Kimsingi, ni wajibu wa msingi kwa wazazi na walezi hukakikisha watoto wanapata haki na mahitaji yao muhimu ili waweze kufurahia maisha kwa kuzingatia kuwa watoto ni kiungo muhimu katika familia na maendeleo ya Taifa.

Serikali kama mdau muhimu wa ustawi na maendeleo ya watoto, inawajibika kuweka mazingira mazuri ya ustawi wa watoto. Aidha, serikali inawajibika kutunga sheria zitakazowalinda watoto ili kesho zao ziweze kutimia na Taifa linufaike kupitia uwepo wao. Ipo changamoto katika jamii zetu kwa baadhi ya wanawake kutupa watoto pindi wanapojifungua watoto hao. 

Wengine huwatupa katika mazingira ambayo ni rahisi kuokotwa na wapita njia lakini baadhi yao huwatupa katika mazingira mabaya mathalani jalalani ambapo kwa bahati mbaya wengine huokotwa wakiwa tayari wameshapoteza maisha. Mbaya sana.

Kwa sababu yeyote ile, suala la kutupa mtoto si suala zuri hasa mtoto anapotupwa katika mazingira mabaya ambayo yanazalisha matatizo mengine mathalani magonjwa kutokana na kupigwa baridi kali na wengine kupoteza maisha kabisa.

 Zipo sababu kadhaa zikiwemo suala la hali ngumu za maisha au baba mzazi wa mtoto kukataa mimba au kumlea mtoto, na hivyo mwanamke kuamua kumtupa mtoto wake aliyehangaika nae kwa miezi tisa tumboni na uchungu wa kumzaa hospitalini.

Januari 17, 2026, karibu na nyumba ya wageni (Guest House) ijulikanayo kwa jina la Kasulu, Nzega Mjini mkoani Tabora, alitelekezwa mtoto ambapo Ofisi ya Mkuu wa wilaya ya Nzega chini ya uongozi wa Mkuu wa wilaya hiyo, Naitapwaki Tukai pamoja na Jeshi la Polisi wilaya ya Nzega waliamua kumchukua mtoto huyo na kumpeleka hospitali kwa uchunguzi na uangalizi huku jitihada za kumpata mama mzazi wa mtoto huyo zikiendelea.

Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kwa upendo mkubwa alionao kwa watoto na jamii, ameamua kumchukua mtoto huyo ambaye amepewa jina la Grace Samia Suluhu Hassan. Tukio hilo la upendo limefanyika Machi 11, 2026, katika makazi yake ya Ikulu ya Chamwino Jijini Dodoma. Kipekee kabisa, nimpongeze Rais Dk. Samia kwa moyo wake wa upendo kwa mtoto huyo kwa kuamua kuchukua jukumu la kumuasili awe ni sehemu ya watoto na familia yake kimalezi na kimatunzo.

Rais Dk. Samia anatoa matumaini mapya juu ya hatma ya mtoto huyo kuwa yupo kwenye mikono salama na Mwenyezi Mungu amjalie mtoto huyo afya njema ili akue vizuri. "Wanaotupa watoto hawajui wanalolifanya. Kuliko kumtupa mtoto ni afadhali ukamkabidhi katika mamlaka za kisheria au kituo cha kulelea watoto. Kila mtoto aliyezaliwa ni hazina na hatujui kesho yake," amesisitiza Rais Dk . Samia.

Pengine ni muda muafaka kwa wanaume kutimiza majukumu ya kimalezi badala ya kutelekeza familia, na hivyo kuwaachia wanawake njia panda, hali inayosababisha baadhi ya wanawake kufikia hatua ya kuwatupa watoto. 

Lakini jambo la muhimu ambalo Rais Dk. Samia amelisisitiza ni kutumia vituo vya watoto kuomba msaada ya kulelewa mtoto badala ya kumtupa mtoto, jambo ambalo si zuri hata mbele za Mungu na hata katika maadili yetu ya Kitanzania. Kwa hakika, Rais Dk. Samia ameonyesha upendo wa kipekee kwa jamii kwa kumuasili mtoto Grace Samia Suluhu Hassan. Tumuombee mtoto Grace Samia Suluhu Hassan awe na afya njema na siku moja aje kuwa nguzo muhimu kwa nchi yetu ya Tanzania.

Dk. Reubeni Lumbagala ni Mwalimu katika Shule ya Sekondari Funguni ya wilayani Pangani mkoani Tanga.

Maoni : 0620 800 462.








Top News