Na Janeth Raphael- MichuziTv

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesisitiza kuwa uhusiano kati ya Tanzania na Rwanda hauishii kuwa wa ujirani tu, bali ni wa kindugu wa kihistoria uliodumu kwa miaka mingi hata kabla ya ukoloni. Amesema kufanana kwa mila, tamaduni na historia ni ushahidi wa undugu huo wa karibu unaowaunganisha wananchi wa mataifa haya mawili.

Akizungumza baada ya mazungumzo rasmi na Rais wa Rwanda, Paul Kagame, aliyefanya ziara ya siku moja nchini Tanzania, Rais Samia alieleza kuwa nchi hizi mbili zimeendelea kushirikiana kwa karibu katika ngazi za kikanda na kimataifa. Ushirikiano huo unajumuisha Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), Umoja wa Afrika (AU), pamoja na Umoja wa Mataifa (UN).

Katika nyanja ya uchumi, Rais Samia alibainisha kuwa biashara kati ya Tanzania na Rwanda imekua kwa kiwango kikubwa, ikifikia thamani ya shilingi bilioni 644 katika mwaka uliopita. Aidha, kuanzia mwaka 1997 hadi Machi mwaka huu, Tanzania imesajili miradi 42 ya uwekezaji kutoka Rwanda yenye thamani ya dola za Marekani milioni 325.5, ambayo imezalisha ajira kwa Watanzania 2,225.

Kwa lengo la kuongeza ukuaji wa uchumi, nchi hizo mbili zimekubaliana kuondoa vikwazo visivyo vya kikodi vinavyokwamisha biashara. Hatua hiyo inalenga kurahisisha matumizi ya soko la pamoja la Afrika Mashariki pamoja na soko huria la bara la Afrika.

Katika sekta ya nishati, Rais Samia alitaja mradi wa pamoja wa kuzalisha umeme katika maporomoko ya Rusumo unaoshirikisha Tanzania, Rwanda na Burundi. Mradi huo una uwezo wa kuzalisha megawati 80 za umeme, na mipango inaendelea kuuzindua rasmi.

Pia, makubaliano yamefikiwa kati ya Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na Shirika la Umeme Rwanda kuanza biashara ya kuuziana umeme, hatua inayotarajiwa kuongeza upatikanaji wa nishati na kuchochea maendeleo ya kiuchumi katika nchi hizo mbili.

Kwa ujumla, ziara hiyo imeimarisha zaidi uhusiano wa kidiplomasia na kiuchumi kati ya Tanzania na Rwanda, huku viongozi wakisisitiza kuendeleza ushirikiano kwa manufaa ya wananchi wao na kanda kwa ujumla.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiongoza Ujumbe wa Tanzania kwenye mazungumzo na Ujumbe wa Rwanda uliongozwa na Rais wa Nchi hiyo Mhe. Paul Kagame, tarehe 03 Mei, 2026.




Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Waandishi wa Habari kuhusu Ziara ya Kikazi ya Rais wa Jamhuri ya Rwanda Mhe. Paul Kagame, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 03 Mei, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Rwanda Mhe. Paul Kagame akizungumza na Waandishi wa Habari kufuatia Ziara yake ya Kikazi Jijini Dar es Salaam, tarehe 03 Mei, 2026


Matukio mbalimbali katika Ziara ya Kikazi ya Rais wa Jamhuri ya Rwanda Mhe. Paul Kagame, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 03 Mei, 2026.


Na Leandra Gabriel, Michuzi TV

SERIKALI Kupitia Wakala wa Majengo Tanzania (TBA,) inatekeleza mradi nyumba za makazi kwa watumishi wa Umma vijana ‘Temeke Kota’ jijini Dar es Salaam kwa gharama ya shilingi Bilioni 21 ikiwa ni sehemu ya kutafuta suluhu ya makazi kwa vijana walioajiriwa katika ofisi za Umma na kufuatiwa na miradi itakayowalenga vijana wasio watumishi wa Umma.

Akizungumza leo mara baada ya kukagua mradi wa ujenzi wa nyumba za makazi kwa vijana watumishi wa Umma wa Temeke Kota Jijini Dar es Salaam Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega amesema; mradi huo wa Nyumba za gharama nafuu una nyumba zitakazobeba familia 144 ambapo nyumba 72 ni chumba kimoja na sebule na choo (studio apartment,) na nyumba 72 ni vyumba viwili pamoja na sebule mahususi kwa wenye familia ndogo.

Waziri Ulega amesema,Serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan suluhu imejizatiti kutafuta suluhu ya nyumba za makazi kwa gharama nafuu na TBA wamekuwa wakifanya jitihada za kina katika kutatua changamoto hiyo kwa makundi mbalimbali wakiwemo vijana.

“Mradi huu umeanza na vijana wanaoanza kazi ya utumishi wa Umma, na kwa maelekezo ya Serikali TBA wataendelea kujenga nyumba za makazi za vijana kwa ujumla, Mpango wa Rais Samia si kwa vijana watumishi pekee bali kwa kundi lote la vijana hivyo waandishi wa habari, wachuuzi na wafanyabiashara watapata fursa ya kupata makazi bora kwa gharama nafuu.” Amesema.

Kuhusiana na gharama za nyumba hizo Ulega amesema; Bei elekezi ni shilingi laki mbili hadi laki tatu na nusu bei zinazoendana na soko na kuitaka Wakala hiyo kuweka mchakato wa wazi katika upatikanaji wa nyumba hizo bila kuhusisha udalali na walengwa wawe vijana na sifa zote ziwekwe wazi kupitia magazeti na mitandao ili vijana walengwa waweze kupata nyumba hizo za Dkt. Samia.

Aidha ameielekeza TBA kutafuta wabia kutoka sekta binafsi na kushirikiana nao katika utekelezaji wa miradi mbalimbali kama Serikali inavyosisitiza ushirikiano baina ya Taasisi za Umma na sekta binafsi katika nyanja mbalimbali.

Kwa upande wake Kaimu Meneja wa TBA Mkoa wa Dar es Salaam Arch. Benard Mayemba amesema kuwa, mradi huo wa ghorofa tisa unatekelezwa kwa Ruzuku kutoka Serikalini umegharimu shilingi Bilioni 21 na hadi sasa takribani shilingi Bilioni 10.2 na unategemewa kukamilika Oktoba 2027.

Aidha amesema; Nyumba hizo zimejengwa kisasa na kuwekwa huduma muhimu kama kisima chenye tanki lenye uwezo wa kuhifadhi maji lita laki tano, lift pamoja na eneo maalum la dharura lililotengwa pindi majanga yanapotokea.

Vilevile Mstahiki Meya wa Manispaa ya Temeke Uzairu Athuman ameishukuru Serikali kupitia TBA kwa kuelekeza mradi huo katika Manispaa hiyo na kuwataka wanufaika kutunza miradi ya namna hiyo kwa kuitumia kwa kadri ilivyopangwa na Serikali.








Rais wa Jamhuri ya Rwanda, Mhe. Paul Kagame amewasili nchini kwa Ziara ya Kikazi ya siku moja yenye lengo la kuimarisha uhusiano wa uwili kati ya Tanzania na Rwanda.

Mhe. Rais Kagame anatarajia kukutana na kufanya mazungumzo  na mwenyeji wake, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Ikulu jijini Dar es Salaam.

Inategemewa kwamba Ziara hii itadumisha mahusiano mazuri na ya kihistoria kati ya majirani hawa wawili. Ushirikiano huu umezidi kuimarika katika miaka ya hivi karibuni kwa kupitia Tume ya Kudumu ya Pamoja (JPC), ambapo Tanzania imeendelea kuwa miongoni mwa washirika wakuu watatu wa biashara wa Rwanda duniani, huku kiwango cha biashara kati ya nchi hizi kikiongezeka kila mwaka. 

Aidha, katika uwekezaji, kuanzia mwaka 1990 hadi Machi 2026, Tanzania imesajili miradi 42 ya uwekezaji kutoka Rwanda yenye thamani ya dola za Marekani milioni 325.53 na kuunda ajira 2,225 katika sekta mbalimbali ikiwemo viwanda, usafirishaji, huduma za kifedha, maliasili na utalii. 

Vilevile, wawekezaji wa Tanzania pia wamewekeza nchini Rwanda kupitia kampuni mbalimbali zikiwemo Bakhresa Group, Magodoro Dodoma, Discount Center, Jambo Plastic, Sagar Enterprises, Buffalo Travelling Tours, Maxcom Africa, Gasabo Grain Milling Company, LCM Delta Company na Metrex Integrated Consultancy.















▪️︎ Asema dini ni nguzo muhimu ya malezi na mshikamano wa Taifa

▪️︎ Asisitiza jamii kuendelea kuombea na kulinda amani ya nchi

Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba, amesema Serikali itaendelea kushirikiana kwa karibu na taasisi za dini nchini ili kuimarisha maadili, mshikamano wa kijamii na kudumisha amani ambayo ni msingi wa maendeleo endelevu ya Taifa.

Amesema hayo leo Jumapili, Mei 3, 2026, aliposhiriki ibada katika Kanisa Kuu la Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Mufindi, lililopo Mafinga Mjini, mkoani Iringa.

Akizungumza na waumini, Dkt. Nchemba amesema taasisi za dini zina mchango mkubwa katika kujenga jamii yenye maadili mema, inayozingatia misingi ya haki na uwajibikaji.

“Serikali inaendelea kusisitiza Watanzania wote kuwa wadau wa kuombea na kusimamia amani ya nchi yetu,” amesema.

Ameongeza kuwa mafanikio ya mipango ya maendeleo ya Taifa yanategemea uwepo wa amani.“Pasipokuwa na amani, hata malengo binafsi ya mtu mmoja mmoja ya Mtanzania mmoja mmoja hayawezi kufikiwa,” amesema.

Waziri Mkuu pia ameeleza mabadiliko ya mazingira ya dunia na changamoto zinazoweza kujitokeza.“Kuna aina mpya ya mapambano, na mapambano hayo ni ya rasilimali na kila palipo na rasilimali mara nyingi huwa kunavutia maadui na hupenda kupitia migawanyiko ya raia wa nchi hizo husika,” amesema.

Katika hatua nyingine, amepongeza juhudi za Kanisa katika malezi ya watoto na vijana.

“Maandalizi ya watoto hivi si tu manufaa kwa Kanisa, ni manufaa pia kwa Taifa tunalolitaka,” amesema.

Kwa upande wake, Askofu wa KKKT Dayosisi ya Mufindi, Dkt. Anthony Kipangula, ameipongeza Serikali kwa kazi ya kuwahudumia wananchi na kusisitiza kuwa ziara za Waziri Mkuu zimeonesha uongozi unaowagusa wananchi moja kwa moja.

“Nimeona juhudi zinazofanywa na Serikali katika kuwajali wananchi mtu wa ngazi yako kushuka mpaka kusikiliza kesi ya mwananchi na kumruhusu ajieleze, niliona ni maajabu kabisa,” amesema.

Ameongeza kuwa Kanisa litaendelea kushirikiana na Serikali katika kuhamasisha maadili mema, kutoa ushauri na kuliombea Taifa ili kudumisha amani na ustawi wa jamii.












Kampuni ya huduma za fedha kidigitali, Mixx, imeendelea kudhihirisha dhamira yake ya kuimarisha uchumi wa wakulima wa karafuu Zanzibar kwa kukabidhi hundi mbili zenye jumla ya shilingi milioni 175 kwa Shirika la Taifa la Biashara Zanzibar (ZSTC).

Akizungumza katika hafla hiyo, Mkuu wa Wilaya ya Mkoani-Pemba, Mhe. Mizza Hassan Faki alisema hatua hiyo ni sehemu ya juhudi endelevu za kampuni katika kuboresha maisha ya wakulima na kuleta mapinduzi katika sekta ya kilimo kupitia suluhisho za kifedha za kidigitali.

Katika makabidhiano hayo, Mixx ilikabidhi hundi ya shilingi milioni 150 kwa ajili ya kugharamia bima ya afya kwa wakulima wa zao la karafuu, hatua inayokamilisha ahadi ya jumla ya shilingi milioni 350 kutoka Mixx kwenda ZSTC. Aidha, hundi nyingine ya shilingi milioni 25 ilitolewa kwa ajili ya ununuzi wa miche 25,000 ya karafuu, ikiwa ni mkakati wa kuendeleza zao hilo muhimu kwa uchumi wa Zanzibar na Tanzania kwa ujumla. Vilevile, hafla hiyo ilishuhudia zoezi la upandaji wa miche ya karafuu, ikiwa ni ishara na dhamira ya pamoja katika kukuza na kulinda zao hilo.

Akielezea umuhimu wa ushirikiano huo, Afisa Mtendaji Mkuu wa Mixx, Bi. Angelica Pesha alisisitiza kuwa ushirikiano wa kimkakati kati ya Mixx na ZSTC umejengwa katika msingi wa kuhakikisha wakulima wanapata huduma bora za kifedha zinazowawezesha kuongeza tija na kipato chao. Alibainisha kuwa kupitia mfumo wa malipo kidigitali wa Mixx, kumekuwa na uwazi, upungufu wa upotevu wa fedha, na kuimarika kwa imani ya wakulima kwa taasisi zinazosimamia sekta hiyo.

“Tunaamini kuwa teknolojia ya kifedha ina nafasi kubwa katika kubadilisha maisha ya wakulima. Kupitia Mixx, tumefanikisha malipo ya haraka, salama na yenye uwazi, na kuondoa changamoto za ucheleweshaji wa malipo zilizokuwepo hapo awali,” alisema.

Kwa mujibu wa takwimu zilizotolewa, katika msimu wa karafuu wa 2025/2026, Mixx kwa kushirikiana na ZSTC imefanikiwa kufanya malipo ya zaidi ya shilingi bilioni 48 kwa wakulima wa Zanzibar. Hatua hiyo pia imechangia kuongezeka kwa ajira, ambapo zaidi ya mawakala 11,000 wamepata ajira na kushiriki katika mnyororo wa utoaji huduma za kifedha.

Aidha, Mixx ilitangaza mipango ya kuanzisha huduma ya mikopo nafuu kwa wakulima wa karafuu, inayotarajiwa kuanza kabla ya msimu wa 2026/2027, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuwawezesha wakulima kuwekeza zaidi katika uzalishaji.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa ZSTC, Ndugu Soud Said Ali, alieleza kuwa ushirikiano na Mixx umeleta mageuzi makubwa katika mfumo wa malipo kwa wakulima, na kuongeza ufanisi katika usimamizi wa zao la karafuu.

Mixx imeendelea kuahidi kushirikiana kwa karibu na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, ZSTC pamoja na wadau wengine ili kuhakikisha sekta ya karafuu inakuwa ya kisasa, yenye tija na endelevu kwa manufaa ya wakulima na uchumi wa Zanzibar kwa ujumla.











Top News