Na Mwandishi Wetu

Serikali ya Kenya imetoa hati rasmi za vyuo vikuu kwa Kenya Advanced Institute of Science and Technology na Kenya Medical Research Institute katika hafla iliyofanyika Ikulu ya Nairobi, hatua inayolenga kuimarisha elimu ya juu, utafiti wa kisayansi na ubunifu nchini humo.

Hatua hiyo imeelezwa kuwa sehemu ya mkakati wa makusudi wa kupanua fursa za elimu ya juu pamoja na kuimarisha mazingira ya utafiti na uvumbuzi yatakayosaidia maendeleo ya taifa.

Kupitia hatua hiyo, Kenya inalenga kujenga mustakabali unaotegemea elimu bora, ubunifu wa ndani na maendeleo endelevu ya tafiti mbalimbali za kisayansi.

Viongozi waliozungumza wakati wa hafla hiyo walisisitiza kuwa vyuo vikuu vina nafasi muhimu katika kuandaa wataalamu wa kada mbalimbali wakiwemo wanasayansi, wahandisi, madaktari na wabunifu ambao watasaidia kuleta mabadiliko ya maendeleo nchini.

Aidha, ilielezwa kuwa pamoja na kuchangia maendeleo ya kitaifa, wataalamu hao pia wanatarajiwa kutoa mchango mkubwa katika nyanja mbalimbali duniani kupitia maarifa, teknolojia na suluhisho za changamoto zinazokabili jamii.

Hatua hiyo pia inatazamwa kama juhudi za Kenya za kuimarisha sekta ya elimu na kuifanya nchi hiyo kuwa kitovu cha utafiti, teknolojia na ubunifu katika ukanda wa Afrika.

Kamati ya Paralympic Tanzania (TPC) kwa kushirikiana na wadau wa michezo ya watu wenye ulemavu, tunatoa pongezi za dhati kwa MR. TUMA DANDI kwa kuchaguliwa kuwa Rais wa Kamati ya Paralympic Tanzania (TPC). 

Tunatambua mchango mkubwa wa International Paralympic Committee pamoja na vyama vyote vinavyosimamiwa na TPC, wadau wa michezo, na mamlaka mbalimbali zinazosimamia maendeleo ya michezo nchini kwa kuendelea kuunga mkono ushirikishwaji, maendeleo na mafanikio ya wanamichezo wenye ulemavu. 

Tunaamini uongozi wako utaendelea kuimarisha mshikamano, maendeleo ya michezo ya Paralympic na kuipeperusha vyema bendera ya Tanzania kimataifa.
*Awataka wananchi kuzitazama vyema fursa zitakazotokana na mashindano hayo kujikwamua kiuchumi

MKUU wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe Albert Chalamila amefanya ziara ya kutembelea ujenzi wa viwanja vya farasi na leaders club wilayani kinondoni ambavyo ni miongoni mwa viwanja vitakavyotumika kwa ajili ya mazoezi wakati wa mashindano ya AFCON na kumtaka mkandarasi kukamilisha ujenzi kwa wakati ambapo ameitaka Halmashauri kuyatumia mashindano hayo kibiashara kwa kuhamasisha utalii lakini pia kutengeneza mazingira wezeshi kwa wananchi kufanya biashara mbalimbali ili kujiongezea kipato

Akizungumza akiwa katika muendelezo wa ziara zake katika Mkoa huo kwenye viwanja vya farasi Wilaya ya Kinondoni Jijini Dar es Salaam RC Chalamila ameitaka Halmashairi hiyo kufanya maboresho ya fukwe zake ikiwemo Coco beach ili ziweze kutumika vyema kuhamasisha utalii wakati wa AFCON huku akishauri kuwepo kwa utalii wa vyakula mbalimbali vya kitanzania hivyo ameitaka Halmashauri kuweka mazingira bora kwa watanzania kufanya biashara ikiwemo ya vyakula

Aidha RC Chalamila ameweeka msisitizo kwenye kukamilika kwa viwanja hivyo kwa wakati ili kumpa heshima Rais Dokta Samia ambae amepata heshima kubwa ya kimataifa ya kuwa mwenyeji wa mashindano hayo ya AFCON

Akiwa katika viwanja vya Leaders RC Chalamila ameelekeza kuimarisha kwa miundombinu ya barabara, upatikanaji wa huduma bora za maji safi na salama lakini pia kuimarishwa kwa mifumo ya ulinzi na usalama ikiwsmo kuwepo kwa taa za barabarani na ametumia nafasi hiyo kuhamasisha usafi na utunzaji wa mazingira.

Kwa upande wa Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni Mhe Saad Mtambule amewahakikishia wananchi kuwa uboreshaji wa viwanja hivyo vya farasi na Leaders Club hautaathiri matumizi ya wananchi ya viwanja hivyo hususani kwa matukio mbalimbali ya kijamii pamoja na mbio za mwendapole ambazo zimekuwa na mchango mkubwa wa kusaidia kukabiliana na magonjwa yasio ya kuambukiza ikiwemo shinikizo la damu na kisukari.






MKUU wa Mkoa wa Ruvuma, Brigedia Ahmed Abbas amewataka wafanyabiashara wa Ruvuma kuwapa ushirikianao waafisa wa TRA watakaopita katika maduka yao ili kuweza kuwapatia elimu ya kodi sambamba na kueleza changamoto zao ili ziweze kutatuliwa.

Ameyasema hayo alipokutana na maafisa wa TRA waliofika ofisi kwake kwa lengo la kumjulisha juu ya uwepo za zoezi la Elimu ya kodi ya mlango kwa mlango wakiongozwa na meneja wa mkoa huo Nicodemas Mwakileme.

Aidha, amewaasa wananchi wa Ruvuma kutojihusisha na biashara ya magendo akisema vitendo hivyo vinaokesesha serikali mapato ambayo yangetumika kujenga vituo vya afya, barabara na mambo mengine kwa maendeleo ya nchi.

Kwa Upande wake, kiongozi wa timu hiyo ya zoezi la Elimu ya kodi mlango kwa mlango Afisa Msimamizi Mkuu wa Kodi Salim Bakari amesema zoezi hilo litaendeshwa kwa wiki mbili katika Wilaya ya Songea, Nyasa, Mbinga na Tunduru yenye lengo la kuwaelimisha wafanyabiashara juu ya mambo mbalimbali ya kodi na kuwahamasisha wananchi wa mipakani kutojihusisha na magendo kwa kuwaelezea athari za magendo na njia sahihi za kuingiza na kutoa bidhaa nchini.

Naye, Kaimu Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wafanyabiashara Mkoa wa Ruvuma, Alhaji Issa Mzee ameipongeza TRA kwa kuja na zoezi hilo kwani litawasaidia wafanyabiashara kueleza changamoto zao ili kuweza kutatuliwa huku akiwasihi kutoa ushirikiano kwa maafisa hao kulipa kodi kwa wakati ili kuweza kujenga vituo vya afya barabara na mambo mengine ya maendeleo.

Mmoja wa wafanyabiashara waliotembelewa na maafisa hao, Olita amesema ameifaidika na elimu hiyo na amejifunza umuhimu wa kutumia mashine za EFD ili kuwa kupata rikodi sahihi za mauzo yao na kusadia kuweza kupata makadirio sahihi ya biashara zao.


Na Mwandishi Wetu
 
Jumuiya ya Tanzania Deejays Community (TDC) imepokea rasmi cheti cha usajili kutoka Baraza la Sanaa la Taifa, hatua inayotajwa kuwa mwanzo wa ukurasa mpya wa maendeleo, umoja na utambuzi wa Ma-DJ nchini.

Akizungumza kuhusu hatua hiyo, Peter More amesema kupatikana kwa usajili huo ni mafanikio makubwa kwa wadau wa tasnia ya u-DJ nchini na kutatoa nafasi ya kuimarisha mshikamano na maendeleo ya sekta hiyo.

Amesema jumuiya hiyo ina matumaini makubwa ya kuendelea kukuza tasnia ya muziki na kuimarisha nafasi ya Ma-DJ katika maendeleo ya sekta ya burudani nchini.

“Tumepewa usajili rasmi na hii ni hatua muhimu inayofungua ukurasa mpya wa umoja, maendeleo na utambuzi wa Ma-DJ nchini,” alisema Dj Peter More.

Aidha, alitoa shukrani kwa Kaimu Katibu Mtendaji wa BASATA, Edward Buganga pamoja na timu nzima ya baraza hilo kwa ushirikiano waliouonyesha katika kufanikisha hatua hiyo.

Dj Peter More alisema Tanzania Deejays Community imeahidi kuwa mabalozi wazuri wa tasnia hiyo kwa kulinda maadili na kuendelea kusaidia juhudi za kukuza ajira kupitia sekta ya muziki na u-DJ.

Alibainisha kuwa safari ya jumuiya hiyo sasa inaanza rasmi kuanzia ngazi ya taifa, mikoa hadi wilaya kwa lengo la kuwafikia Ma-DJ wengi zaidi nchini na kuimarisha maendeleo ya tasnia hiyo.

Na Mwandishi Wetu

Serikali ya Kenya imezindua rasmi kampeni ya kugombea nafasi ya Jaji wa International Criminal Court kwa kipindi cha mwaka 2027 hadi 2036 kwa Justice Njoki Ndung’u, hatua inayolenga kuiwakilisha nchi hiyo katika taasisi ya kimataifa ya utoaji haki.

Uzinduzi huo ulifanyika katika Ikulu ya Nairobi, ambapo Jaji Njoki Ndung’u alisifiwa kwa mchango wake mkubwa katika sekta ya sheria na haki, ndani na nje ya Kenya.

Akiwa mmoja wa majaji wanaoheshimika nchini Kenya, Jaji Njoki amewahi kuhudumu katika Bunge la Kenya, Bunge la Afrika pamoja na taasisi za United Nations, jambo lililompa uzoefu mpana katika masuala ya sheria ya kimataifa, haki za binadamu na mfumo wa haki ya jinai.

Aidha, ameelezwa kuwa ameonyesha uwezo mkubwa wa kitaaluma katika sheria, uhuru wa kiakili, ujasiri katika kufanya maamuzi na kujitolea katika kusimamia haki na uwajibikaji katika majukumu yake ya kitaifa na kimataifa.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa wakati wa uzinduzi huo, Jaji Njoki anatajwa kuwa na mchanganyiko wa sifa muhimu ikiwemo mamlaka ya kimahakama, uadilifu, uzoefu wa kutunga sheria pamoja na uelewa wa masuala ya kimataifa unaoendana na mahitaji ya ICC katika juhudi zake za kupambana na ukwepaji wa haki duniani.

Hatua hiyo inatajwa kuwa sehemu ya juhudi za Kenya kuendelea kushiriki katika kuimarisha taasisi za sheria na haki katika ngazi ya kimataifa.
 






















Na Byera Deus

Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) limeanza kulipa fidia kwa wananchi 280 wa kata nne za Wilaya ya Karagwe wanaopitiwa na mradi wa kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 220 kutoka Benaco hadi Kyaka, kufuatia maagizo yaliyotolewa Mei 9, 2026, na Waziri wa Nishati, Deogratias Ndejembi, wakati wa ziara yake mkoani Kagera.

Mhandisi anayehusika na masuala ya kuchora ramani na kupima ardhi katika mradi huo kutoka Makao Makuu ya TANESCO, Derick Kaijanangoma, alisema jumla ya shilingi bilioni 1.7 zimetolewa kwa ajili ya ulipaji fidia katika awamu ya kwanza kwa wananchi wa kata za Nyaishozi, Nyakahanga, Bugene na Nyakasimbi.

Alisema gharama za mradi za kulipa fidia ni shilingi bilioni 6.1, na Serikali imeanza kutoa fedha kwa wananchi wote wanaopisha ujenzi wa mradi huo katika wilaya za Ngara, Karagwe na Missenyi.

“Zoezi la ulipaji fidia tayari limefanyika katika Wilaya ya Ngara na sasa linaendelea katika maeneo ya Karagwe. Tunajua kwamba tathmini ilifanyika mwaka 2022, lakini sasa muda wa kulipwa fidia umefika, na kila familia itafikiwa. Hata kama muhusika amepoteza maisha, kama nyaraka zimetimia na vigezo vimezingatiwa, atapatiwa haki yake,” alisema Kaijanangoma.

Alisema kuwa baada ya kulipwa fidia, wananchi hawataruhusiwa kuendelea kufanya shughuli zozote za kibinadamu katika maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya mradi, na wametakiwa kuondoa mali zao ndani ya siku 30, huku uwezekano wa kuongezewa muda ukiwepo pale inapobidi ili kumpa nafasi mkandarasi kuendelea na kazi.

Alitoa wito kwa wananchi waliopokea fidia kuhakikisha wanarudisha kilekile kilichofidiwa, kama ni ardhi, nyumba au misitu, na wasitumie fedha hizo katika masuala mengine kama kuongeza mke au kukimbia familia.

Sarafina Gasiliel, Afisa Maendeleo ya Jamii wa mradi huo, alisema changamoto kubwa ambazo wamekutana nazo katika ulipaji wa fidia ni migogoro ya ndoa, migogoro ya ardhi ambayo tayari imethaminishwa pamoja na ukosefu wa elimu ya mirathi.

Alitoa wito kwa wananchi kumaliza migogoro kwanza ili fidia ijulikane inaenda kwa nani, huku wananchi wote waliopoteza ndugu zao waliopaswa kulipwa fidia wakitakiwa kupata msimamizi wa mirathi atakayeweza kupokea fidia hiyo kwa niaba ya wanafamilia wa marehemu.

Kwa upande wao, baadhi ya wananchi akiwemo mkazi wa Kijiji cha Bisheshe, Fidelix Banyesige, wameishukuru Serikali na TANESCO kwa kuanza kulipa fidia licha ya kuchelewa kwake tangu walipofanyiwa tathmini mwaka 2022.

“Tunalishukuru shirika kwa kutulipa fidia. Ingawa imechelewa, tuko tayari kupisha mradi huu kwa manufaa ya wananchi wengine ambao bado hawajapata huduma ya umeme,” alisema Banyesige kwa niaba ya wananchi hao.

Mradi huo wa kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 220 unatarajiwa kuboresha upatikanaji wa huduma ya umeme katika maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Kagera na kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii.









Na Said Mwishehe,Michuzi TV 

DIWANI wa Kata Kariakoo Haji Manara ametoa ombi malaamu kwa Baraza la Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam pamoja na Mkurugenzi wa Jiji hilo kuja na ajenda maalum ya kuhakikisha Dar es Salaam inakuwa safi kuelekea michuano ya AFCON.

Tanzania na hasa Jiji la Dar es Salaam imepewa heshima ya kuwa mwenyeji wa ufunguzi wa michuano ya AFCON hivyo matarajio kutakuwa na maelfu ya wageni kutoka mataifa mbalimbali,hivyo kuwa na ajenda ya kudumu kwa ajili ya kuliboresha Jiji hilo ni muhimu ikawa ya kudumu kuanzia sasa.

Akiwasilisha maombi maalum katika Kikao cha Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam kilichofanyika leo Mei 14,2026 ,Manara ametumia nafasi hiyo kuzungumzia hatua zinazopaswa kuchukuliwa na Mkurugenzi wa Jiji na Meya kuhakikisha Jiji linakuwa safi.

“Mungu akitujaalia mwakani Tanzania  itakuwa mwenyeji michuano ya AFCON na ufunguzi utanyika jijini Dar es Salaam na kutakuwa na mechi zitakzochezwa Dar es Salaam.Hivyo naomba tuwe na ajenda ya kudumu itakayokuwa inajadili kwa kushirikiana na kamati ya maandilizi na serikali yetu

“Sura ya Dar es Salaam inaendelea kupendeza lakin lazima tufanye jitihada za kuhakikisha Jiji linakuwa safi kwani itakuwa aibu kuwa na Jiji  chafu,mitaro kujaa maji, lakini kuwa na misongamano isiyokuwa na ulazima.

“Pia kuelekea AFCON lazima tuandae watu wa kupokea wageni,hivyo Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Sslaam nakuomba ubebe ajenda hii.Jiji la Dar es Salaam kuna Hoteli zenye hadhi ya Five Star tano ambazo zinaweza kupokea maelfu ya wageni.”

Akifafanua zaidi Manara amesema pamoja na uwepo wa hoteli hizo iko haja kwa Mkurugenzi pamoja na Meya kuangalia uwezekano wa kuzungumza na wamiliki wa Apatiment ili ziweze kupokea wageni kwani wapo watakaotoka mikoani ambapo sio wote wanaweza kufikia kwenye hoteli kubwa,hivyo watafikia kwenye apatimenti ziliozopo.

“Naomba tuzungumze na wamiliki wa Apatiment kwa ajili ya kupokea wageni,kwani sio watu wote ambao wataweza kukaa Hayat Regency na hoteli nyingine kubwa za namna hiyo, hivyo wengine watakaokuja watakaa huko,”amesema Manara.

Wakati huo huo amesema kwa upande mwingine Jiji la Dar es Salaam limekuwa nyuma katika utalii hivyo iko haja ya kuwa na kumbi maalum ambazo zitakuwa zinatumika katika utalii katika kipindi ambacho michuano ya AFCON itakuwa inaendelea.







Na Said Mwishehe,Michuzi TV

MEYA wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam Nurdin Bilali maarufu Shetta amesema anatambua na kupongeza kazi nzuri inayofanywa na Baraza la madiwani pamoja na watumishi wote wa halmashauri hiyo.

Aidha amesema kutokana na ushirikiano baina ya viongozi wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam ni wazi wataendelea kutekeleza majukumu yao na kubwa zaidi ni kuifanya halmashauri hiyo kuwa namba moja nchini katika kukusanya mapato.

Akizungumza katika kikao cha Baraza la Mdiwani Robo 3 ya mwaka 2026 kuanzia Januari hadi Machi katika Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam kilichokutana kujadili taarifa za utendaji kazi wa kata za Halnashauri ya Jiji la Dar es Salaam.

“Naomba kutambua kazi nzuri inayofanywa na kila mmoja wetu katika halmashauri yatu na viongozi wa kitaifa wamekuwa wakipongeza baraza letu kwa kazi nzuri inayofanyika,ukweli tunapokea sifa nyingi.

“Tuendelee kuwa halmashari namba moja katika kukusanya mapato,kufanya kazi kwa bidii na hatimaye kuilete heshima nchi yetu pamoja na kumletea heshima Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Rais Dk.Samia Suluhu Hassan.

Katika kikao hicho pia Baraza la Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam limeshuhudia Diwani Mteule wa Viti Maalum Gema Ishengoma akila kiapo cha kuwa Diwani ambapo Meya Bilal ametumia nafasi hiyo kumkaribisha huku akiomba madiwani na watumishi wa Jiji hilo kumpatia ushirikiano ili aweze kutimiza majukumu yake kwa maendeleo ya wananchi.

“Chama Cha Mapinduzi(CCM)kama kilivyokuwa ltanuru la kupika viongozi kuanzia jumuiya ya chipukizi basi hata diwani aliyekuja atatusaidia katika baraza la halmashauri na kubwa zaidi tutampa ushirikiano ili apate nafasi ya kufanya kazi vizuri









Top News