Na Janeth Raphael MichuziTv 

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Ridhiwani Kikwete, amesema Serikali itaendelea kutoa motisha kwa watumishi wa umma kupitia upandishaji wa vyeo kwa wale wenye sifa na wanaokidhi vigezo vilivyowekwa, huku akisisitiza umuhimu wa nidhamu ya kazi, uzalendo na uwajibikaji katika kulitumikia taifa.

Kikwete ameyazungumza hayo leo jijini Dodoma wakati akifungua wiki ya utumishi wa uma mkoani humo ambapo amesema 

kuhusu maendeleo ya Utumishi wa Umma, Serikali inaamini kuwa watumishi ndiyo nguzo muhimu ya maendeleo ya nchi, hivyo kuendelea kuwawezesha kutachangia kuongeza ufanisi wa utoaji huduma na kuchochea maendeleo ya taifa kwa ujumla.

“Tunapowajengea uwezo na kuwapa motisha watumishi wa umma, tunakuwa si tu tumewawezesha wao binafsi, bali pia tumekomboa taifa kupitia huduma bora kwa wananchi,” alisema.

Aidha, amewataka watumishi kuendelea kutumia mifumo ya kisasa ya utendaji kazi iliyowekwa katika Utumishi wa Umma ili kuhakikisha kunakuwa na utendaji wenye tija, uwajibikaji na matokeo chanya kwa taasisi, sekta mbalimbali na taifa kwa ujumla.

Ameeleza kuwa kwa sasa mifumo hiyo imeunganishwa na taratibu za upandishaji vyeo pamoja na kuthibitishwa kazini, hatua inayolenga kuongeza uwazi na ufanisi katika usimamizi wa rasilimali watu serikalini.

Waziri huyo pia ametoa maelekezo kwa watumishi wote wa umma kutekeleza majukumu yao kwa uwazi, uaminifu, weledi na ufanisi ili kuondoa malalamiko yasiyo ya lazima kutoka kwa wananchi na kuongeza imani kwa Serikali.

“Ninapenda kusisitiza kuwa wafanyakazi wetu ndiyo msingi wa maendeleo yetu. Mkitekeleza wajibu wenu kwa uadilifu na kujituma, mafanikio makubwa na maendeleo tunayoyatarajia kama Watanzania yatafikiwa,” alisema.

Katika hatua nyingine, Ridhiwani amesema Serikali imekamilisha zoezi la kuhuisha miundombinu ya maendeleo ya kada mbalimbali za Utumishi wa Umma zilizo chini ya wizara na taasisi zake. Maboresho hayo yamehusisha kuingizwa kwa fani mpya zinazozalishwa na vyuo vikuu na taasisi za elimu ya juu ambazo awali hazikuwa zimejumuishwa katika mifumo hiyo.

Amebainisha kuwa maboresho hayo yamegusa kada zote muhimu, ikiwemo sekta za afya, elimu, sheria, uhandisi, kilimo, mifugo, teknolojia ya habari na mawasiliano (TEHAMA), nishati pamoja na maeneo mengine muhimu ya maendeleo.

Hatua hiyo, kwa mujibu wa Waziri, inalenga kuifanya Serikali kuwa na mfumo wa Utumishi wa Umma unaokwenda sambamba na mabadiliko ya teknolojia, mahitaji ya soko la ajira na vipaumbele vya maendeleo ya taifa.





TAKUKURU Mkoa wa Geita imefikisha mahakamani watumishi 9 wa umma kwa tuhuma za kutumia vibaya na kuiba fedha za umma kiasi cha shilingi milioni 89,055,107 na senti 50. 

Watumishi hao walikamatwa baada ya uchunguzi wa TAKUKURU kubaini walikuwa wakifanya vitendo vya rushwa na ubadhirifu. Kati yao watumishi 3 wa Manispaa ya Geita walikuwa wakikusanya mapato ya Serikali kupitia mfumo wa LGRCS lakini walikwepa kutoa stakabadhi na kutumia mashine za POS. Pesa zote zilizokusanywa hazikufika Serikalini na jumla ya shilingi milioni 48,067,500 ilipotea.

Wengine 4 ni watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Geita ambao walirudishia fedha za Mahakama Kuu Masjala Ndogo Geita kisha wakazitaka tena kwa njia ya rushwa kupitia simu na miamala ya benki. Kiasi kilichotumika vibaya hapo ni shilingi milioni 41,987,607 na senti 50.

Watumishi wengine 2 kutoka Idara ya Utafit iwa Madawa Mwanza na Hospitali ya Rufaa Bugando pia walishirikiana nao. Baada ya kukamilisha uchunguzi na kupata vibili kutosha, washtakiwa wote wamefunguliwa mashtaka 4 mahakamani tarehe 17 Juni 2026 na kesi zao zinasikilizwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Geita.

Mkuu wa TAKUKURU Geita Ndugu Said Lipandaje amesema hatua hiyo inaonyesha Serikali imedhamiria kupambana na rushwa bila woga.




Na Mwandishi Wetu, Morogoro

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano Deus Sangu amesema mahusiano mema, mazungumzo ya kujenga na mshikamano wa kitaifa ni nguzo muhimu katika kuimarisha demokrasia, amani na maendeleo endelevu nchini.

Akifungua Warsha ya Viongozi wa Vyama vya Siasa na Wajumbe wa Baraza la Vyama vya Siasa leo Juni 17, 2026, mjini Morogoro, Waziri Sangu alisema Serikali itaendelea kushirikiana na wadau wote wa kisiasa kwa kuzingatia misingi ya kuheshimiana, ushirikishwaji na kutanguliza maslahi ya Taifa.

Alisema viongozi wa vyama vya siasa wanapaswa kuwa mstari wa mbele kuhamasisha mazungumzo yenye kujenga, kudumisha amani na kuimarisha mshikamano wa kitaifa badala ya kuhimiza migogoro.

“Mahusiano mema ndiyo msingi wa amani, umoja na maendeleo ya Taifa. Tunaposhirikiana kwa heshima na maelewano bila kujali tofauti zetu za kiitikadi, tunajenga Taifa imara lenye mshikamano,” alisema Waziri Sangu.

Aidha, aliwataka viongozi hao kushirikiana na Serikali katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 itakayoanza kutekelezwa Julai Mosi, 2026, akieleza kuwa mafanikio ya dira hiyo yanategemea ushirikiano wa wadau wote wa maendeleo bila kujali tofauti za kisiasa.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Baraza la Vyama vya Siasa nchini, Juma Ali Khatibu alisema uwepo wa vyama vya siasa unatoa mchango mkubwa katika kuimarisha mahusiano na mshikamano ndani ya jamii.

Pia alimpongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kumteua Dkt. Eveline Munisi wa Chama cha NCCR-Mageuzi kuwa Mbunge na Naibu Waziri katika Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, akisema hatua hiyo ni ishara ya kuendelea kuimarika kwa ushirikiano na maridhiano ya kisiasa nchini.

Wakati huo huo  Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Mstaafu Francis Mtungi, alisema warsha hiyo ilitokana na uamuzi wa Kikao cha Kamati ya Utendaji ya Baraza la Vyama vya Siasa kilichofanyika Mei 21, 2026, ambapo ilikubaliwa Ofisi ya Waziri Mkuu iandae mada kuhusu jukumu jipya la mahusiano kwa lengo la kujenga uelewa miongoni mwa wadau wa kisiasa.

Katika wa Warsha kuhusu Dhana ya Mahusiano na Ushirikishwaji, Bw.Rasheed Maftah Mkurugenzi wa Idara ya Mahusiano amelezea kuhusu Dhana ya Mahusiano,wadau husika, Misingi yake na majukumu ya Viongozi wa Siasa katika kuimarisha Mahusiano mema katika jamii.

Aidha, alieleza pia kuhusu Majukumu ya Idara ya Mahusiano katika luteleleza jukumu jipya la Ofisi la kuratibu Mahusiano baina ya Serikali na Makundi ya Kijamii.

Warsha hiyo imewakutanisha viongozi wa vyama vya siasa 18 kati ya 19 vyenye usajili kamili kutoka Tanzania Bara na Zanzibar, ikiwa ni sehemu ya jitihada za Serikali kuendelea kuimarisha mahusiano, mazungumzo na ushirikiano kati ya vyama vya siasa kwa ajili ya kudumisha amani, umoja na maendeleo ya Taifa.

Vyama vya Siasa vilivyoshiriki ni CCM, CUF,UMD, NCCR-Mageuzi, NLD, UPDP, NRA,ADA TADEA, TLP,UDP,MAKINI, SAU,AAFP, CCK, ADC,CHAUMA na ACT Wazalendo.




Na Mwandishi Wetu

HALIMASHAURI ya Wilaya ya Kisarawe,Mkoani Pwani imeendelea kung'ara kwa kupata hati safi kutoka Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serkali (CAG), kwa kipindi cha miaka minne mfurulizo.

Wilaya hiyo imepata hati safi katika mwaka wa fedha 2021/22 , mwaka wa fedha 22/23, mwaka wa fedha 23/24 na mwaka huu wa fedha wa 24/25.

Akizungumza katika kikao maalumu cha Baraza la Madiwani la halmahauri hiyo, Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Mhe Abubakar Kunenge, amewapongeza viongozi wa wilaya na halimashauri hiyo kwa uwajabikaji.

Kunenge amesema hati safi hizo ziwe chachu kwa wilaya na halimashauri hiyo kutekeleza mikakati ya maendeleo na kupunguza changamoto za wananchi.

Ameeleza, hati safi ni lazima iakisi maendeleo yaliyopo katika halimashauri hivyo kuwataka viongozi na watendaji kuongeza nguvu katika kubuni vyanzo vya vipya vya mapato,ukusanyaji wa mapato na uwekezaji.

"Hati safi inatokana na ukaguzi wa hesabu za fedha zilivyo tumika kwa usahihi, hivyo Kisarawe ni lazima sasa mjielekeze katika kupanga bajeti ya kutekeleza mirdi ya maendeleo,"amesema Kunenge.

Amesema, Kisarawe inatakiwa kufanya jitihada kubwa za kuinuka kiuchumi kwani ina fursa nyingi zinazo vutia uwekezaji.

"Naomba tu ni wachane, Kisarawe kuna changamoto ya migogoro ya ardhi. Unaleta wawekezaji lakini wanakimbia kwa sababu ya migogoro.Malizeni migogoro yenu," amesema

Amebainisha Kisarawe inafursa za utalii na uchmbaji madini unaoweza kuvuta ujenzi wa viwanda hivyo kuongeza mapato.

"Mjiulize kwanini watu wanachimba madini hapa lakini hawajengi viwanda.Ondoeni migogoro.Madiwani msiogope kueleza wazi kuhusu wavamizi wa ardhi katika maneno yenu,"ameeleza Kunenge.

Mwenyekiti wa Baraza la Halimashauri ya Wilaya ya Kisarawe, Aidan Kitare, alimhakishia mkuu huyo wa mkoa kuwa Halmashauri hiyo inamikakati kabambe ya kujikwamua kiuchumi, ikiwemo uwekezaji katika ardhi na usimamizi wa vyanzo vya mapato.

Mkaguzi wa Nje kutoka Ofisi ya CAG Mkoa wa Pwani, Faith Mutune, ameipongeza halmashaurihiyo kwa kupata hati safi na kuitaka kufunga hoja nane za ofisi hiyo zilizo salia.

Awali Mweka Hazina wa halmashauri hiyo ,Grace Maembe, alieleza utekelezaji wa hoja za CAG kwa mwaka 2024/25 kuwa zilikuwa 29, ambapo hoja 19 zimetekelezwa sawa na asilimia 66%, hoja nane zinaendelea kutekelezwa sawa na asilimia 28%, hakuna hoja isiyo tekelezwa, hoja mbili zimejirudia hivyo kufanya halmashauri hiyo kutekeleza kwa asiliomia 100 ya hoja zote za CAG.











Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), kupitia Idara ya Mambo ya Ndani (INAD), leo Juni 17, 2026 imeandaa Kongamano la Maadili lililowakutanisha viongozi wa dini mbalimbali kujadili nafasi ya maadili katika kuimarisha ukusanyaji wa kodi na kujenga utamaduni wa ulipaji kodi kwa hiari. Kongamano hilo ni sehemu ya maandalizi ya Maadhimisho ya Miaka 30 ya TRA yatakayofanyika Julai 1, 2026.

Akifungua kongamano hilo kwa niaba ya Kamishna Mkuu wa TRA, Naibu Kamishna wa TRA, Bw. Mcha Hassan Mcha, amesema kuwa katika kipindi cha miaka 30 tangu kuanzishwa kwa TRA, taasisi hiyo imepiga hatua kubwa katika kuimarisha mifumo ya ukusanyaji wa mapato, huku maadili yakiendelea kuwa nguzo muhimu katika utekelezaji wa majukumu yake.

Bw. Mcha amesema TRA inaendelea kuwekeza katika mifumo na mikakati mbalimbali ya kuimarisha maadili kwa watumishi wake na walipakodi ili kujenga uaminifu, uwajibikaji na kuongeza kiwango cha ulipaji kodi kwa hiari.

“Maadili hujenga imani, na imani hujenga ulipaji wa kodi kwa hiari,” alisema Bw. Mcha.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Maridhiano Tanzania (JMAT), Sheikh Alhad Mussa Salum, ameipongeza TRA kwa kuandaa kongamano hilo na kueleza kuwa maadili ni msingi muhimu wa maendeleo ya jamii na taifa. Amesema mafundisho ya dini yanasisitiza uadilifu, uwajibikaji na kufanya mema, huku ulipaji wa kodi ukiwa sehemu ya wajibu unaochangia ustawi wa wananchi na maendeleo ya nchi.

Naye Mkuu wa Evangelical Fellowship Church Tanzania, Askofu Charles Asher Howard, amesema maandiko matakatifu yanaelekeza waumini kutimiza wajibu wao kwa mamlaka halali, ikiwemo kulipa kodi. Amebainisha kuwa maendeleo ya Tanzania yanategemea mchango wa kila mwananchi, hivyo ulipaji wa kodi ni jukumu la pamoja linalopaswa kutekelezwa kwa uaminifu na uzalendo.

Viongozi hao wa dini wamepongeza hatua ya TRA ya kuwashirikisha katika mijadala ya maadili na ukusanyaji wa mapato, wakisisitiza kuwa ushirikiano kati ya taasisi za umma na viongozi wa dini una nafasi muhimu katika kuhamasisha wananchi kulipa kodi kwa hiari na kujenga taifa lenye uwajibikaji, uadilifu na maendeleo endelevu.
















Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) imeandika historia nyingine baada ya jopo la madaktari bingwa na wataalamu wa afya kufanikisha salama uzazi wa watoto watano kwa wakati mmoja kwa Bi. Victoria Mkwizu, mkazi wa Tabata jijini Dar es Salaam. Watoto hao wamezaliwa tarehe 13 Juni 2026 na wanaendelea vizuri chini ya uangalizi wa wataalamu wa hospitali hiyo, ambapo watatu ni wa kiume na wawili ni wa kike.


Akiwa wodini, Bi. Victoria amesema anafurahia huduma alizopata katika Hospitali ya Taifa Muhimbili tangu alipopokelewa hadi kujifungua salama watoto hao watano. Amewapongeza madaktari, wauguzi na wataalamu wengine wa afya kwa uangalizi wa karibu waliompatia katika kipindi chote cha matibabu, akieleza kuwa mchango wao umewezesha yeye na watoto wake kuendelea vizuri. 

Kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili, Mkurugenzi wa Huduma za Upasuaji, Dkt. Rachel Mhaville amesema tukio hilo ni la kipekee na limehitaji ufuatiliaji wa karibu kutoka kwa timu ya wataalamu wa hospitali hiyo ili kuhakikisha usalama wa mama na watoto huku akimpongeza Bi. Victoria kwa kujifungua salama watoto hao watano na kuwatakia afya njema.

Aidha Dkt. Mhaville amesema Muhimbili itagharamia gharama zote za matibabu za Bi. Victoria na watoto wake kuanzia alipolazwa hospitalini tarehe 15 Mei 2026 hadi watakapomaliza matibabu na kuruhusiwa kurejea nyumbani. Amesema hatua hiyo ni sehemu ya jitihada za hospitali kuhakikisha mama na watoto wanaendelea kupata huduma bora na salama katika kipindi hiki muhimu.









Na. Ssgt Mawazo Mtondo - Dodoma.

Mkuu wa Sehemu ya Usimamizi wa Maadili na Ushughulikiaji wa Malalamiko (Mrejesho) wa Jeshi la Polisi, Naibu Kamishna wa Polisi (DCP) Adolphina Ngoso, Mkuu wa Kitengo cha Utumishi wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, Naibu Kamishna wa Zimamoto na Uokoaji (DCP) Fatma Ngenya na Mkuu wa Kitengo cha Mafunzo  Idara ya Uhamiaji, Naibu Kamishna wa Uhamiaji (DCI) Bahati Mwaifuge kwa nyakati tofauti, leo Juni 17, 2026 wametembelea Banda la Maonesho la Jeshi la Magereza lililopo katika Viwanja vya Chinangali Park jijini Dodoma.

Viongozi hao walifanya ziara hiyo katika Maadhimisho ya Kitaifa ya Wiki ya Utumishi wa Umma 2026 yanayoendelea kufanyika Jijini Dodoma, ambapo walipata fursa ya kujionea huduma mbalimbali, shughuli za urekebishaji wa wafungwa, pamoja na kazi za uzalishaji mali zinazotekelezwa na Jeshi la Magereza kupitia Programu mbalimbali za urekebishaji.

Kwa nyakati tofauti, wageni hao walipokelewa na Mkuu na Msemaji wa Jeshi la Magereza katika Maonesho ya Mwaka huu, Kamishna Msaidizi wa Magereza (ACP) Elmas L.Mgimwa, ambaye aliwaeleza majukumu ya Jeshi la Magereza katika Usalama, mchango wake katika utoaji wa huduma za urekebishaji na mageuzi yaliyopo sasa katika utekelezaji wa majukumu yake yanayochsngia kwa kiasi kikubwa maendeleo nch kijamii na kiuchumi.





Waziri wa Kilimo, Mhe. Daniel Chongolo (Mb), amekutana kwa mazungumzo na ujumbe ulioongozwa na Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Frontier, Bw. Lars Tushuizen tarehe 11 Juni 2026, jijini Dodoma ambao wana nia ya kuwekeza katika Sekta ya Kilimo.

Mazao hayo ni Parachichi na Chai ambapo wamejadili kuimarisha uzalishaji, kuongeza thamani na kupanua wigo wa masoko ya ndani na nje ya nchi kwa manufaa ya wakulima na maendeleo ya Sekta ya Kilimo nchini.

Bw. Lars Tushuizen ameeleza kuwa Kampuni yake inalenga kuendeleza mnyororo wa thamani wa mazao hayo kupitia uwekezaji wa matumizi ya teknolojia za kisasa. Ameeleza kuwa amevutiwa kuwekeza nchini kwa kuwa Tanzania ina mazingira mazuri ya uwekezaji na fursa kubwa za uzalishaji wa Parachichi na Chai, ambapo fursa hizo zinaweza kuchangia kuongeza mapato ya wakulima na ukuaji wa uchumi wa Taifa.

Mhe. Waziri Chongolo amekaribisha uwekezaji na kuahidi kuwa Serikali itatoa ushirikiano kwa wawekezaji hao na wengine wowote wenye dhamira ya kuendeleza Sekta ya Kilimo nchini. Amesisitiza kuwa Wizara ya Kilimo itaendelea kuweka mazingira wezeshi yatakayovutia wawekezaji, kuimarisha ushindani wa mazao yanayozalishwa Tanzania katika masoko ya Kimataifa ili kuleta tija kwa wakulima na Taifa kwa ujumla.

Washiriki katika Mkutano huo walikuwa ni Mha. Athumani Kilundumya, Naibu Katibu Mkuu anayesimamia Umwagiliaji na Zana za Kilimo; Prof. Peter L. M. Msoffe, Naibu Katibu Mkuu anayesimamia Maendeleo ya Mazao na Usalama wa Chakula; Bi. Beatrice Banzi, Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Chai Tanzania; wakiwemo Maafisa Waandamizi wa Wizara ya Kilimo.


📍Ampongeza Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kuboresha barabara nchini


Na Mwandishi Wetu, Mbeya.

SERIKALI imewagiza mameneja na wahandisi wa TANROADS na TARURA nchini kutumia mifumo mipya ya kielektroniki kulinda hifadhi za barabara na kutekeleza miradi kwa viwango.

Agizo hilo limetolewa Jijini Mbeya Leo Juni 17 2026 na Mkuu wa Wilaya ya Mbeya, Mhe. Solomon Itunda, wakati akimwakilisha Mkuu wa Mkoa huo, Mhe. Beno Malisa, kufungua mafunzo ya viongozi wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) na Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA).

Mafunzo hayo ya siku nne yaliyoanza Jumatatu, Juni 15, 2026, yamewakutanisha Mameneja, Wahasibu, na Wahandisi kutoka mikoa ya kimkakati ya kiuchumi ikiwemo Mbeya, Songwe, Rukwa, Ruvuma, Mtwara, na Lindi.

Teknolojia na Udhibiti wa Miundombinu

Mhe. Itunda amebainisha kuwa lengo kuu la semina hiyo ni kuwajengea uwezo viongozi hao katika kusimamia miradi ya miundombinu kwa ufanisi, hasa kupitia matumizi ya mfumo mpya wa kielektroniki unaodhibiti na kusimamia matumizi holela ya hifadhi za barabara nchini.

Alitumia jukwaa hilo kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kumwaga mabilioni ya fedha katika ujenzi wa barabara, hatua iliyoleta mageuzi makubwa ya kijamii na kiuchumi.

"Serikali inaendelea kuhakikisha kuwa barabara zinajengwa na kuboreshwa ili kufungua fursa za kiuchumi kwa wananchi. Tunampongeza Mheshimiwa Rais Samia kwa juhudi hizi kubwa, na nitoe wito kwenu washiriki kutumia mafunzo haya kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yenu," alisisitiza Mhe. Itunda.


Mapinduzi ya Kiuchumi vijijini

Pia, DC Itunda amewahimiza washiriki kutumia ipasavyo maarifa hayo ya kidijitali kuhakikisha utekelezaji wa miradi unazingatia viwango na taratibu zilizowekwa kiofisi bila kuwa na changamoto zozote.

Kitalamu, mafunzo haya yanatarajiwa kuwa chachu ya kuimarisha ushirikiano kati ya taasisi hizo mbili (TANROADS na TARURA), kuongeza uwajibikaji, na kurahisisha usafirishaji wa bidhaa za kilimo na biashara katika ukanda wa Nyanda za Juu Kusini na taifa kwa ujumla.







Na Clement Robert, WAF - Dodoma

Tanzania imeeleza utayari wake wa kuunga mkono juhudi za kukabiliana na mlipuko wa ugonjwa wa Ebola unaoendelea katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) na Uganda kwa kutoa vifaa tiba, vifaa kinga kwa wahudumu wa afya pamoja na wataalamu wenye uzoefu katika kudhibiti milipuko ya magonjwa.

Kauli hiyo imetolewa leo Juni 16,2026 na Waziri wa Afya Mhe. Mohamed Mchengerwa kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, wakati wa Mkutano wa Ngazi ya Juu wa Wakuu wa Nchi na Serikali pamoja na wadau uliojadili hatua za kukabiliana na mlipuko wa virusi vya Ebola aina ya Bundibugyo katika nchi hizo mbili.

Amesema, Tanzania imeeleza mshikamano wake na serikali pamoja na wananchi wa DRC na Uganda, huku ikitoa pole kwa familia zilizopoteza wapendwa wao kutokana na ugonjwa huo na kuwatakia nafuu ya haraka wagonjwa wote walioathirika.

“Tanzania tumeendelea kuimarisha uwezo wa kujiandaa na kukabiliana na milipuko ya magonjwa kupitia uwekezaji katika mifumo ya ufuatiliaji wa magonjwa, uchunguzi katika maeneo ya mipakani, maabara, vifaa tiba na mifumo ya mwitikio wa haraka, huku tukijidhatiti na kujna umuhimu wa ushirikiano wa kikanda na bara zima”

Mhe. Mchengerwa ameongeza, kwa kuitaka Africa CDC pamoja na nchi wanachama kuimarisha zaidi uratibu, kuwekeza katika mifumo ya maandalizi na mwitikio wa haraka, na kuhakikisha rasilimali zinapatikana kwa wakati ili kudhibiti mlipuko wa sasa, kuzuia majanga yajayo na kujenga Afrika yenye afya na usalama zaidi.

 Aidha, Tanzania imepongeza juhudi za Rais wa Burundi, Mheshimiwa Ndayishimiye, Tume ya Umoja wa Afrika, Kituo cha Afrika cha Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa (Africa CDC) na Shirika la Afya Duniani (WHO) kwa uratibu na uongozi wao katika kuitisha mkutano huo na kusimamia hatua za mwitikio dhidi ya mlipuko huo.






Top News