Na: Dk. Reubeni Lumbagala

Utunzaji wa Mazingira ni jukumu letu sote. Uwe mtoto, kijana, mtu mzima au mzee. Uwe mwanamke au mwanamme, uwe msomi au usiwe msomi, suala la utunzaji mazingira linakuhusu. Faida za utunzaji mazingira zinatunufaisha sote. Madhara ya uharibifu mazingira yanatuathiri sote. Hakuna aliye salama mazingira yakiharibika. Ndiyo maana ni vyema mikakati ya utunzaji mazingira ikafanyika mapema.

Dunia kwa sasa inakabiliwa na changamoto ya mabadiliko ya tabianchi. Kutokana na changamoto hiyo, mikakati inawekwa ya namna bora ya kukabiliana na changamoto hiyo ili kuifanya dunia kuwa mahali salama pa kuishi na kufurahia maisha. Tanzania kwa kuwa si kisiwa, tumeathirika pia na mabadiliko ya tabianchi kama zilivyo nchi nyingine. Serikali imechukua hatua kadhaa ikiwemo suala la kuhamasisha watu binafsi, taasisi, makampuni na wizara kupanda miti ili kupunguza athari.

Rais Dk. Samia Suluhu Hassan amekuwa mfano mzuri wa kuigwa kuanzia kuhamasisha watu kupanda miti hadi kufanya kwa vitendo yeye mwenyewe kupanda miti. Tangu akiwa Makamu wa Rais, Dk. Samia kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais - Muungano na Mazingira hadi sasa amekuwa Rais kamili, anaendelea kuhimiza sana utunzaji mazingira na kupanda miti kwa maendeleo. 

Hata katika kuadhimisha Siku yake ya kuzaliwa (Birthday) Januari 27, 2026, Rais Samia aliitumia siku hiyo kupanda miti. "Sisi tulirithi uoto wa asili mwingi sana, tulirithi nchi yetu ambayo haikuwa imeharibika kiasi hiki. 

Tulirithi miti mingi ya matunda iliyopandwa shambani na mingine kujiotea. Lakini leo mtoto wetu akitaka kula pera lazima akalinunue sokoni. Sisi tulikuwa tunapita msituni na kula mapera ya aina yoyote tunayotaka," amesema Rais Dk. Samia.

Baraza la Mitihani Tanzania (NECTA) kama taasisi ya elimu iliyo chini ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, nayo imeunga mkono juhudi za kutunza mazingira kwa kuweka mpango wa kupanda miti ipatayo 150,000 katika taasisi mbalimbali za elimu kama shule za msingi, sekondari na vyuo vya ualimu nchi nzima. 

Machi 18, 2026, Katibu Mtendaji wa NECTA, Prof. Said Mohamed, alizindua zoezi la kitaifa la upandaji miti katika Shule ya Sekondari Makutupora ya Jijini Dodoma ambapo katika shule hiyo, miti 600 imepandwa kufuatia agizo ya Rais Dk.Samia kwa NECTA katika maadhimisho ya miaka 50 ya NECTA. Prof Said amesema "Desemba 16, 2023, Rais Dk. Samia alikuwa mgeni rasmi katika maadhimisho ya miaka miaka 50 ya NECTA alitupa maagizo ya kupanda miti kwa sababu sisi ni watumiaji wa karatasi ambazo zinazalishwa na miti, hivyo tunapanda miti kuunga mkono jitihada za utunzaji mazingira."

Mkakati wa NECTA wa kupanda miti 150,000 katika taasisi mbalimbali za elimu utachangia kwa kiasi kikubwa jitihada za kuiokoa nchi yetu na madhara ya mabadiliko ya tabianchi. Lakini pia miti hiyo itasaidia kupendezesha mandhari za shule na vyuo na kufanya sehemu hizo kuwa vutivu kwa ufundishaji na ujifunzaji wa maarifa, stadi na ujuzi. 

Hakika nawapa kongole NECTA kwa kuratibu mkakati huu mzuri wa kupanda miti katika taasisi za elimu. Kwa mwaka 2023/2024, NECTA walipanda miti 82,676, mwaka 2024/2025 walipanda miti 110,400 na kwa mwaka 2025/2026, lengo ni kupanda miti 150,000. Muhimu ni wanufaika wa shule zitakazopata miche ya miti, kuitunza kikamilifu miti hiyo kwa manufaa endelevu.

Maoni 0620 800 462.






Na Mwandishi Wetu, Pangani

Katibu wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) wilaya ya Pangani mkoani Tanga, Nasri Mkalipa, ameanza ziara ya kuimarisha uhai wa Chama na kusikiliza kero za wananchi, ziara iliyopewa jina la "Operesheni Samia."

Mkalipa ameanza ziara hiyo Machi 24, 2026, katika Kata za Mkalamo na Mkwaja ambapo ameonana na makundi mbalimbali ya kijamii ikiwa ni utaratibu wa CCM wa kuwafikia wananchi kule walipo, kusikiliza na kutatua kero zao kwa wakati.

Akiwa ziarani humo, Mkalipa amewaasa vijana kujiunga katika vikundi ili kunufaika na mikopo ya asilimia kumi inayotolewa na Halmashauri. "Vijana wenzangu tujiunge katika vikundi ili tuweze kunufaika na mikopo. Rais wetu na Mwenyekiti wa CCM Taifa, Dk. Samia Suluhu Hassan anatoa fedha nyingi za mikopo, ni jukumu letu vijana kuchangamkia fursa hizo," amesema Mkalipa. 

Sambamba na hilo, Mkalipa amewaeleza vijana kujiandaa kwa ujio wa mashindano ya mpira wa miguu yaliyopewa jina la Aweso Vijana Cup. Katika hatua nyingine, Mkalipa amesema CCM ni Chama imara kinachoaminika na wananchi wake kutokana na sera zake nzuri zinazogusa maisha ya wananchi. Ziara hiyo ya siku tisa itazifikia Kata zote Kumi na Nne za wilaya ya Pangani.









Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeeleza kufurahishwa na ushirikiano wa kimatibabu kati ya Hospitali ya Benjamin Mkapa na Chuo Kikuu cha Tiba cha Vienna, huku ikikaribisha upanuzi wa ushirikiano huo katika taasisi nyingine za kibobezi ikiwemo Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) na Taasisi ya Saratani ya Ocean Road (ORCI), kwa lengo la kuboresha huduma za afya nchini.

Hayo yameelezwa na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayeshughulikia masuala ya nje, Mhe. Ngwaru Maghembe (Mb), akimwakilisha Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo (Mb), katika mazungumzo ya kidiplomasia na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Austria anayeshughulikia masuala ya kisiasa, Mhe. Balozi Dkt. Hannah Liko, yaliyofanyika Machi 24, 2026 katika ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam.

Katika mazungumzo hayo, Mhe. Maghembe amepongeza mchango wa Austria katika sekta ya elimu, ikiwemo utoaji wa mikopo yenye masharti nafuu na utekelezaji wa miradi ya kujifunza kwa njia ya mtandao (e-learning) visiwani Zanzibar kupitia kampuni ya eeeAustria GmbH. Ameiomba Austria kuongeza nafasi za masomo ya uzamili na uzamivu kwa Watanzania, hususan katika nyanja za Teknolojia ya Habari, kilimo na utalii.

Aidha, amekaribisha mpango wa Global Gateway wa Umoja wa Ulaya (EU) kama nyenzo muhimu ya kuhamisha ushirikiano kutoka misaada ya jadi kuelekea uwekezaji wa kimkakati na biashara. Pia ameeleza azma ya kuandaa Jukwaa la Biashara na Uwekezaji katika robo ya pili ya mwaka 2026 ili kutangaza fursa zilizopo chini ya Dira ya Maendeleo ya 2050.

Kwa upande wake, Dkt. Liko amesisitiza utayari wa Austria kuendelea kushirikiana na Tanzania licha ya changamoto za siasa za kimataifa. Amesema Austria itaendelea kushirikiana na Tanzania katika sekta ya utalii kupitia kubadilishana uzoefu na wataalamu, pamoja na kuonesha nia ya kusaidia miradi mbalimbali ikiwemo ya nishati.

Katika mazungumzo hayo Tanzania imeihimiza Austria kufungua ubalozi mkazi nchini ili kurahisisha uratibu wa miradi ya maendeleo.
















Waziri wa Fedha na Mipango, Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) akiwa kwenye picha ya pamoja na wenyeviti wa Bodi na Wakurugenzi wa Mashirika na makampuni ambayo serikali ina hisa chache kwenye mkutano wa mwaka 2026 uliyofanyika jijini Arusha , waliosimama wa kwanza kulia , ni Meneja Mkazi wa Barrick nchini , Dkt. Melkiory Ngido

Waziri wa Fedha na Mipango, Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) akiwa kwenye picha ya pamoja na wenyeviti wa Bodi na Wakurugenzi wa Mashirika na makampuni ambayo serikali ina hisa chache kwenye mkutano wa mwaka 2026 uliyofanyika jijini Arusha , waliosimama wa kwanza kulia , ni Meneja Mkazi wa Barrick nchini , Dkt. Melkiory Ngido.

Waziri wa Fedha na Mipango, Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) kwenye mkutano huo.

Sehemu ya washiriki wa mkutano huo.

Sehemu ya washiriki wa mkutano huo.


**
Serikali imeendelea kutambua mafanikio yanayoendelea kupatikana kutokana na ubia baina ya kampuni ya Barrick na Serikali ya Tanzania kupitia kampuni ya Twiga ambapo katika mkutano wa Wakurugenzi wenye Hisa chache za Serikali (MIF 2026) uliomalizika jijini Arusha imetunukiwa tuzo ya mshindi katika kipengele cha uwakilishi bora wa Bodi za Wakurugenzi (MIF) Directors Forum 2026 Outstanding Board Representation) na ofisi ya Msajili wa Hazina.

Barrick -Twiga imekuwa kinara wa kuendesha shughuli zake kwa kufuata sheria za madini , kanuni za nchi na kwa uwazi ambapo imefanikisha kuendesha shughuli za uchimbaji wa madini nchini kwa mafanikio sambamba na kuweza kuchangia Pato la Taifa na kunufaisha wananchi kupitia miradi mbalimbali ya kijamii inayotekelezwa kupitia migodi yake ya North Mara,Bulyanhulu na Buzwagi ambao uko katika mchakato wa kufungwa.

Mkutano huo uliowakutanisha wakurugenzi wa Bodi,Watendaji Wakuu,Watunga sera na wataalamu mbalimbali ulikuwa jukwaa la kujadili changamoto za uendeshaji na kuweka mikakati ya kuboresha utendaji wa kampuni ambazo Serikali ina hisa chache.

Katika mkutano huo ,Meneja Mkazi wa Barrick nchini,Dkt. Melkiory Ngido, alifanya wasilisho kuhusu kufikiri upya uendeshaji wa shughuli za madini kwa manufaa katika kipindi hiki cha mpito cha kimkakati katika sekta ya madini sambamba na kuwa na mifumo imara inayoweza kutekelezeka katika siku za usoni na inayoweza kusimamiwa kwa ufasaha na viongozi wa bodi.

Katika kipengele cha mabadiliko katika mazingira ya uchimbaji madini nchini aligusia masuala mbalimbali ya kuangalia kwa umakini kama vile mahitaji, siasa za kijiografia, umakini katika hatua mbalimbali kwenye tasnia kama vile kwenye uchimbaji na usindikaji na bei tete za bidhaa.

Pia aligusia masuala ya mnyororo wa thamani, kuongeza mauzo ya nje ,udhibiti wa biashara, kukidhi matarajio ya jamii kunufaika na shughuli za madini na kukidhi mahitaji ya wawekezaji.

Kuhusu suala la kufikiri upya undeshaji wa shughuli za madini kwa manufaa aligusia masuala ya athari zinazoweza kujitokeza katika uwekezaji katika tasnia ya madini nchini ikiwemo kubadilisha kanuni, kukithiri kwa uanaharakati, upotoshaji wa taarifa, siasa za kikanda na masuala endelevu.

Dkt. Ngido aligusia suala la kuimarisha mifumo kama vile kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi, huduma za maji na umeme,huduma za kimtandao ,kukuza mnyororo wa thamani wa kimataifa, teknolojia na umuhimu wa kuwa na uongozi unaotoa maamuzi kwa haraka ,kuchochea ukuaji, kujenga uaminifu na kutatua matatizo kwa haraka.

Alisema katika uendeshaji wa shughuli za madini kwa weredi baadhi ya mambo yanayopaswa kuzingatiwa aliyataja kuwa ni utekelezaji wa malengo Endelevu ya Umoja wa Mataifa, kushirikiana na wadau wa nje wenye utaalamu zaidi, kushirikisha jamii, kuweka wazi mgawanyo wa mapato, kuimarisha miundombinu, huduma za umeme na jinsi ya kurithishana ujuzi na kujenga kizazi cha wataalamu wa siku zijazo.

Kuhusu matarajio ya baadaye yanayopaswa kutazamwa katika uboreshaji wa sekta ya madini Dkt. Ngido alisema ni sera, kanuni, sheria masharti ya kutoa leseni , maslahi ya taifa, kuaminiana na kuwa na mawasiliano mazuri na taratibu nzuri za utatuzi wa migogoro.

Akihitimisha wasilisho lake katika mkutano huo, Dkt. Ngido alisema kuna umuhimu wa kuwa na mifumo katika migodi kwa njia ya uwazi,nidhamu na ushirikiano thabiti na mifumo hiyo isiwekwe kwa njia ya dharura.

Akiongea katika mkutano huo,Msajili wa Hazina, Bw. Nehemiah Mchechu alisema ofisi yake itaendelea kuhakikisha kampuni ambazo Serikali ina hisa chache zinaendeshwa kwa ufanisi, zinatoa faida endelevu na zinachangia kikamilifu katika ajenda ya maendeleo ya muda mrefu ya nchi.


Na John Mapepele

Waziri wa Afya, Mheshimiwa Mohamed Mchengerwa amesema Tanzania leo, Machi 24, 2026 imeungana na mataifa mengine duniani kuadhimisha Siku ya Kifua Kikuu Duniani, siku maalum inayolenga kuongeza jitihada za kupambana na ugonjwa huu hatari unaoendelea kuathiri mamilioni ya watu duniani.

Amewataka watanzania kuendelea kushirikiana na Serikali ili kutokomeza ugonjwa huo hapa nchini.

"Ili kuhakikisha tunafanikiwa kutokomeza ugonjwa huu, jitihada za pamoja za wadau wote katika kuwajibika zinahitajika." Amesisitiza Mhe. Mchengerwa

Aidha, katika tamko rasmi lililotolewa na Mganga Mkuu wa Serikali, Dkt. Grace Magembe, Serikali imesisitiza umuhimu wa ushirikiano wa pamoja katika kufanikisha azma ya kutokomeza kifua kikuu ifikapo mwaka 2030.

Kauli mbiu ya mwaka huu, “Kwa Jitihada za Pamoja za Viongozi, Wadau na Wananchi, inawezekana Kutokomeza Kifua Kikuu nchini,” imebeba ujumbe mzito wa uwajibikaji kwa kila mmoja.

Kauli hii inalenga kuwakumbusha viongozi, wadau wa maendeleo pamoja na wananchi kuwa mapambano dhidi ya kifua kikuu yanahitaji mshikamano na mchango wa pamoja, ikiwemo uwekezaji wa rasilimali kutoka ndani ya nchi.

Licha ya ugonjwa huu kubaki kuwa miongoni mwa magonjwa hatari ya kuambukiza, Tanzania imepiga hatua kubwa katika kupunguza maambukizi mapya.

Kwa mujibu wa takwimu za Shirika la Afya Duniani (WHO) za mwaka 2024, visa vya kifua kikuu vimepungua kwa asilimia 44—kutoka wagonjwa 306 kwa kila watu 100,000 mwaka 2015 hadi 172 kwa mwaka 2024. 

Aidha, vifo vinavyotokana na ugonjwa huo vimepungua kwa asilimia 59, kutoka vifo 56,000 hadi 23,500 katika kipindi hicho.

Mafanikio haya yanachangiwa na uwekezaji wa Serikali katika sekta ya afya, hasa kuboresha miundombinu ya uchunguzi na upatikanaji wa dawa.

Serikali pia imehakikisha wagonjwa wanapatiwa matibabu bila malipo na kufuatiliwa ili kuhakikisha wanamaliza dozi, hatua muhimu katika kuzuia usugu wa dawa.

Hata hivyo, pamoja na mafanikio hayo, bado juhudi zinahitajika ili kufikia lengo la kutokomeza ugonjwa huu ifikapo mwaka 2035.

Serikali imeendelea kuhamasisha wananchi kujitokeza kupima mapema wanapopata dalili kama kikohozi cha muda mrefu, homa za mara kwa mara, jasho la usiku au kupungua uzito.

Aidha, jamii imetakiwa kuondoa unyanyapaa dhidi ya wagonjwa wa kifua kikuu na badala yake kuwapa msaada wa kijamii na kisaikolojia. 



Dkt. Magembe amesisitiza kuwa mgonjwa anapoanza matibabu hupunguza uwezekano wa kuambukiza wengine, hivyo ushirikiano wa jamii ni muhimu katika kudhibiti maambukizi.

Katika kukabiliana na ugonjwa huu, wananchi pia wanahimizwa kuzingatia tahadhari kama kuepuka msongamano usio wa lazima, kuhakikisha maeneo yenye hewa safi na kutoa taarifa mapema kwa wahudumu wa afya kuhusu watu wenye dalili.

Serikali, chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, imeahidi kuendelea kuboresha huduma za afya hadi ngazi ya jamii ili kuhakikisha kila mwananchi anapata huduma bora kwa wakati.

Serikali inatoa wito kwa Watanzania wote kuchukua hatua ambapo kwa kufanya hivyo kutasaidia kutokomeza kifua kikuu na kulinda afya ya vizazi vya sasa na vijavyo.
NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

BARAZA la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam pamoja na wadau wa mazingira, linatarajia kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Kupunguza Taka “Taka Sifuri” kwa kutoa elimu kwa wananchi juu ya mbinu za kubadilisha taka kuwa malighafi au bidhaa nyingine, hatua inayolenga kuifanya taka kuwa fursa ya kiuchumi.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Machi 24, 2026, Meneja wa Uzingatiaji wa Sheria wa NEMC, Hamadi Kissiwa, amesema maadhimisho hayo yatafanyika kuanzia Machi 28 hadi Machi 30, 2026 katika viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam.

Amesema kaulimbiu ya kimataifa ya maadhimisho hayo ni “Wezesha taka sifuri kwenye sekta ya chakula”, huku kaulimbiu ya kitaifa ikiwa ni “Taka ni Fursa”. Ameongeza kuwa mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Hamad Masauni.

Kissiwa amefafanua kuwa lengo kuu la maadhimisho hayo ni kubadilisha mtazamo wa jamii kuhusu taka, kwa kuhamasisha matumizi ya dhana ya 3Rs ambayo ni Kupunguza (Reduce), Kutumia tena (Reuse) na Kurejeleza (Recycle), ili kuongeza ufanisi katika matumizi ya rasilimali na kupunguza uchafuzi wa mazingira.

Amesema matumizi ya mbinu hizo yatasaidia kupunguza kiwango cha taka kinachotupwa ovyo, huku yakichangia upatikanaji wa malighafi kwa ajili ya uzalishaji wa bidhaa nyingine, hali itakayosaidia kukuza uchumi wa mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla.

Aidha, ameeleza kuwa maadhimisho hayo pia yanalenga kuangazia changamoto ya upotevu wa chakula duniani, ambapo takwimu zinaonesha kuwa utupaji wa chakula unachangia takribani asilimia 10 ya uzalishaji wa hewa chafuzi, hali inayochangia mabadiliko ya tabianchi na kuathiri ustawi wa jamii.

Mbali na hilo, Kissiwa amewakaribisha wananchi na wadau wa mazingira kushiriki kikamilifu katika maadhimisho hayo yatakayofanyika kuanzia saa 12 asubuhi hadi saa 11 jioni, yakijumuisha maonesho ya fursa za uwekezaji katika sekta ya usimamizi wa taka pamoja na ubunifu wa bidhaa zitokanazo na taka.

Amesisitiza kuwa ushiriki wa wananchi ni muhimu katika kufanikisha ajenda ya “taka sifuri”, ambayo inalenga kujenga jamii inayotambua thamani ya taka na kuzitumia kama rasilimali badala ya kuziona kama uchafu.









Mrajis wa Vyama vya Ushirika, Dkt. Benson Ndiege amevitaka Vyama vya Ushirika vya Mazao nchini kutumia mizani za kidigitali katika kupima mazao ya wakulima ili kuondoa udanganyifu na kumlinda mkulima.


Mrajis ametoa maelekezo hayo kupitia barua ya tarehe 13 Machi, 2026 aliyowaandikia Wenyeviti na Wajumbe wa Bodi wa Vyama vya Ushirika vya mazao Tanzania Bara kuhakikisha kuwa vinatumia mizani za kidigitali kwa lengo la kuondoa udanganyifu kwenye upimaji wa mazao ya wakulima na kurahisisha upatikanaji wa takwimu sahihi za makusanyo/mauzo ya mazao.

Vyama vya Ushirika wa Mazao vitakavyobainika kuwa na Mizani ya kidijitali na havitumii Mizani hizo au kuzitumia kwa matumizi tofauti na malengo yaliyokusudiwa, vitachukuliwa hatua kwa mujibu wa Sheria; na wakulima wanatakiwa kuhakikisha mazao yao yanapimwa kwa kutumia Mizani zilizounganishwa na Mfumo wa Usimamizi wa Vyama vya Ushirika (MUVU) ili kuwawezesha kupata malipo stahiki ya mazao yao.

Aidha, Dkt. Ndiege amevitaka Vyama vyote vya Ushirika wa Mazao ambavyo bado havijatekeleza maelekezo ya ununuzi wa Mizani za kidijitali kuhakikisha kuwa vinanunua Mizani hizo kwa kufuata utaratibu wa manunuzi na Mwongozo wa Ofisi ya Mrajis kuhusu Ununuzi wa Mizani hadi kufikia Juni 31, 2026.

Tume ya Maendeleo ya Ushirika inaendelea na jitihada za kuimarisha Usimamizi wa Vyama vya Ushirika nchini ambapo kwa sasa moja ya kipaumbele kinachotiliwa mkazo ni kuratibu na kuhimiza Vyama vya Ushirika vya Mazao, kuweka utaratibu wa ununuzi wa Mizani za Kidijitali sambamba na matumizi sahihi ya mizani hizo.

MFUMO wa stakabadhi ghala umetajwa kuboresha masoko ya mazao kwa wakulima na kuwafanya kupata tija na kutambuliwa na taasisi za kifedha zinawawezesha kupata mikopo mbalimbali.

Mfumo huo umeweza kuwasaidia wakulima kutolanguliwa mazao yao na watu wa kati ‘madalali wa mazao na kupelekea wakulima kupata tija ya mazao yao.

Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB), Asangye Bangu, amesema kuwa mfumo huu umeimarika “mfumo sasa umeimarika tunatekeleza kwenye mikoa 23 kati ya mikoa 26 ya Tanzania bara na tuna bidhaa 18 zinazopita kwenye mfumo huu tija sasa inaonekana waziwazi”

Amesema kuwa tija hiyo inaonekana kwa wazalishaji mali yaani wakulima na kwa Halmashauri katika kukusanya tozo zao.

Amesema kuwa Mfumo unafanya ukusanyaki kupitia vyama vya ushirika, wakusanyaji wengine ni wafanyabiashara wenye leseni za kufanya biashara huko nyuma walikuwa wanatambulika kama madalali lakini sasa wananuzi hawa wananunua kwa bei ya sokoni kwa kuwa zinatolewa kwa uwazi.

Amesema kuwa mazoa hayo yakiingizwa gharamani huwekwa kwenye kazidata ya bodi ya stakabadhi ghalani, “kazidata hiyo ndio inayotumika na wenzetu wa soko la bidhaa na ukizungumza na sisi basi lazima uzungumze na pacha wetu muuzaji soko la bidhaa Tanzania, wao wanauza mazoa yao kidigitali na kusema kweli tumefaidika na tumeona umuhimu wa kutumia mfumo huu tukishirikiana na wamiliki wa mazao kama mazao yenye bodi basi tunashirikiana na bodi hizo lakini kwa yale mazao yasiyokuwa na bodi basi sisi tunashirikiana na Mamlaka ya udhibiti wa nafaka na mazao mchanganyiko”.

“Kwa umoja wetu tunaweza kuhakikisha mkulima yule na lile zao lake alililolitolea jasho anakwenda sokoni akirejea na tija zaidi,”alisema Bangu.

Bangu amesema kuwa tayari zao la korosho kupitia mfumo huo kwa limeuzwa kiasi cha zaidi ya tani 400,000. Na Mbaazi zaidi ya tani 200,000, ufuta tani 200,000, na sasa zao la Choroko linaendelea kuuzwa ambapo kwa sasa zishauzwa tani 60,000, .

“Unaweza kuona hata yale mazoa hayakuwahi kutegemewa kama mazoa ya kibishara sasa yanakuza uchumi wa mkulima,”amesema Bangu.

Amesema sasa wakulima wamekuwa wanatambulika na taasisi za kifedha jambo ambalo linamewahahakikisha kupata mikopo, “kimsingi tumerasmisha biashara ya mazoa”.

Bangu amesema kuwa mfumo huo unatoa ajira “kwenye kila ghala ukitoa mmiliki wa ghala kunakuwa na wafanyakazi watano pale nimekuwa nikishuhudia vijana wanaomaliza vyuo vikuu na kuja kujiunga na sekta ikiongezeka,”.

Amesema kuwa mfumo huo upo kwenye mikoa hiyo 23 na kuwashauri wakulima wote kupitisha mazao yao kwenye mfumo huo .

Bangu amesema kuwa bodi hiyo inaendelea kuwekeza kwenye maghala ya ndani na kuziingiza kwenye mifumo maghala mapya ikiwa pamoja na kuhakikisha kuwa soko la ndani linaendelea kuleta tija.

Amesema kuwa jukumu la kudhibiti ubora wa bidhaa na mazao bodi hiyo imelikabidhi kwa msimamizi wa ghala ambaye anajukumu la kuhakikisha kuwa hakuna bidhaa au zao litakaloingia likiwa halina ubora naye atahakikisha mnunuzi naye anachukua bidhaa yenye ubora.

Amesema kuwa wakulima hawalazimishwi kuuza mazao yao kwa mfumo wa stakabadhi ghalani lakini kwa yale mazao yenye bodi ni lazima mazao hayo yaratibiwe na bodi husika.

Amewakaribisha wadau mbalimbali wa kilimo na stakabadhi ghalani kwenye maadhimisho ya miaka 20 ya kuanzishwa kwa mfumo huo ambapo kutakuwa na maonesho katika ukumbi wa Jakaya Kikwete jijini Dodoma kuanzia tarehe 28 mpaka 30 Aprili mwaka huu.

Akielezea kuanzishwa kwa mfumo huo amesema kuwa ulianzishwa baada ya kubainika kuwa hiyo ndio njia itakayomaliza changamoto za soko kwa wakulima na kuhakikisha kilimo kinakuwa kina tija.

“Kimsingi mfumo huu ulianza kufanyiwa utafiti tangu 2000 ulipoonekana unaweza kuwasaidia wakulima na wazalishaji mbali maana ulionekana unaweza kufanya kazi kwa wakulima na pia kwa wazalishaji wengine ambao sio wakulima.

“Katika kuliona jambo hili na faida yake basi mwaka 2006 ikanzisha bodi ambapo sheria ilitungwa 2005 na kanuni ziliaanza 2006 na taasisi ikaanza kipindi hicho hicho kuanzia hapo mfumo ukaanza katika hatua tofauti tofauti kama mtoto kuna nyakati za kutembea, kusimama na kukimbia anavyokuwa na niwashukuuru Watanzania kwa kuendelea kuonesha nia ya kuutumia mfumo huo.

Kwa upande wake David Sukali, Mkuu wa kitengo cha Manunuzi bodi ya usimamazi wa Stakabadhi za ghala, amesema kupitia mfumo huo umewawezesha wakulima kupata mikopo na nafuu zote za kifedha.

Akizungumzia manufaa ya mfumo huo Sukali amesema kuwa “Mfumo huu unamanufaa makubwa unapotumika hususani katika mazao tukiinza na zao la korosho mathalan kwenye bei na wanunuzi kupata uhakika wa mazao,

Mbali na hilo amesema kuwa mfumo huo umewezesha wakulima kuwa karibu na soko na hivyo kurahisha kuuza mazoa kwa bei yenye tija na kwa haraka,
Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi ghala (WRRB) Asangye Bangu



Mwenyezi Mungu akitaka jambo litokee  hutokea ndivyo ilivyotokea, uumbwaji wa Kasoko ya Ngorongoro zaidi ya miaka milioni 2.5 iliyopita ambapo mlima mrefu uligeuzwa kuwa bonde la Ngorongoro.

Wanafunzi wa madrasa kutoka jimbo la Kondoa mkoani Dodoma pamoja na walimu wao wameshuhudia uwezo huo wa Mwenyezi Mungu walipotembelea hifadhi ya Ngorongoro katika ziara iliyoandaliwa na mbunge wa jimbo hilo mheshimiwa Dkt Ashatu Kijaji (Mb)

Afisa Mhifadhi Mkuu na mkuu wa makumbusho ya Urithi Geopark Dkt. Agnes Gidna aliwaeleza wanafunzi na waalimu hao kuwa mlipuko mkubwa wa volcano uliugeuza mlima mkubwa uliokuwepo eneo hilo  zaidi ya miaka milioni 2.5 iliyopita na kuwa kreta hii ni kudhihirisha wazi kwamba kwa Mungu hakuna kubwa.

Akizungumza kwa niaba ya kamishna wa Uhifadhi wa Mamlaka hiyo, Kamishna Msaidizi Mwandamizi Gloria Bideberi amempongeza mbunge wa jimbo hilo Dkt. Ashatu Kijaji ambaye pia ni waziri wa maliasili na Utalii kwa kusimamia sekta hiyo kwa vitendo ambapo ujio wa wanafunzi hao utaongeza jitihada za kutangaza utalii wa ndani.

Kiongozi wa Ujumbe huo Katibu wa Idara ya Elimu ofisi ya mbunge wa jimbo la Kondoa Ayoub Sogoi amesema ziara hiyo imedhihirisha kwa vitendo mafunzo wanayopata vijana hao kutoka madrasa na shule za msingi na sekondari.









VUNJO.

MBUNGE wa Jimbo la Vunjo mkoani Kilimanjaro, Enock Koola ameendelea na ziara yake ya kuhamasisha kilimo cha kahawa katika jimbo hilo ambapo mamia ya wakulima wakijitokeza kushiriki na kupata elimu kuhusu mbinu bora za uzalishaji wa zao hilo la kimkakati.

Katika mwendelezo wa ziara hiyo, Mbunge pamoja na timu yake ilitembelea kata za Mwika Kaskazini na Mamba Kaskazini, akiambatana na Mbunge wa Viti Maalum, Dkt. Catherine Joachim pamoja na Mkuu wa Wilaya ya Moshi, Godfrey Mnzava kuhamasisha wakulima wa zao la kahawa.

Akizungumza na wananchi, Koola alisisitiza umuhimu wa kufufua na kuimarisha kilimo cha kahawa kama nguzo kuu ya uchumi wa wananchi wa Vunjo.

Alibainisha kuwa juhudi za pamoja kati ya serikali, viongozi wa kisiasa na wakulima ni msingi wa kuongeza uzalishaji, kuboresha ubora wa kahawa, na kuhakikisha wakulima wanapata masoko yenye tija.

Kwa upande wake, Dkt. Catherin Joachim aliwahimiza wakulima kuchangamkia fursa zilizopo katika sekta ya kahawa kwa kuzingatia ushauri wa wataalamu wa kilimo na kutumia mbinu za kisasa ili kuongeza tija na kipato.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Moshi, Mnzava, alisisitiza umuhimu wa ushirikiano kupitia vyama vya ushirika pamoja na matumizi sahihi ya pembejeo ili kuongeza ushindani wa kahawa ya Vunjo katika soko la ndani na kimataifa.

Wakulima wamepongeza jitihada za Mbunge kwa kushirikiana na Serikali katika kuhakikisha zao la kahawa linakuza uchumi wa kaya na maendeleo ya jamii katika eneo hili.






Top News