MKUU wa Wilaya ya Handeni, Salum Nyamwese,akizungumza wakati wa maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yaliyofanyika katika Halmashauri ya Mji Handeni chini ya kaulimbiu isemayo “Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana; Msingi Jumuishi kufikia Dira 2050.”

Na Mwandishi Wetu

MKUU wa Wilaya ya Handeni, Salum Nyamwese, amesema Rais Samia Suluhu Hassan amedhamiria kuwatua ndoo kichwani wanawake wa Handeni kupitia utekelezaji wa mradi wa maji wa miji 28 ambao umefikia zaidi ya asilimia 75 ya utekelezaji.

Mradi huo unaogharimu Dola za Marekani 81,142,931 unatekelezwa na mkandarasi M/s Jwil Infra Limited kutoka India na unatarajiwa kuhudumia zaidi ya wakazi 870,629 kutoka vijiji 161 vya wilaya za Handeni, Korogwe, Muheza na Pangani.

Nyamwese ametoa kauli hiyo wakati wa maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yaliyofanyika katika Halmashauri ya Mji Handeni chini ya kaulimbiu isemayo “Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana; Msingi Jumuishi kufikia Dira 2050.”

Amesema mradi huo utakuwa mkombozi kwa wanawake ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakitumia muda mwingi kutafuta maji.

“Niwahakikishie msikae kinyonge mkajiona nyie ni dhaifu. Serikali imewasikia na tatizo hili la maji litatatuliwa hivi karibuni… hata yale mnayosema kina mama wanashindwa kusuka nywele vizuri kwa sababu ya maji, watasuka na tutawaona,” amesema.

Nyamwese amesema serikali chini ya uongozi wa Rais Samia imeendelea kuweka mazingira rafiki ya kumuwezesha mwanamke kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo kupitia sera, sheria na mipango mbalimbali.

Amebainisha kuwa Rais Samia pia alitoa maelekezo ya kuboreshwa kwa utoaji wa mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na halmashauri kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu baada ya kubaini awali kulikuwa na changamoto katika utoaji wake.

“Mheshimiwa Rais alielekeza halmashauri kuweka utaratibu mzuri wa utoaji wa mikopo hii ili kuhakikisha makundi haya yanapata fursa ya kujikwamua kiuchumi,” amesema.

Ameongeza kuwa Wilaya ya Handeni imeendelea kushuhudia maendeleo ya wanawake katika shughuli za kiuchumi zikiwamo ujasiriamali, kilimo na ufugaji.

Kuhusu kupambana na ukatili wa kijinsia, Nyamwese amesema serikali inaendelea kutoa elimu kwa jamii ili kuheshimu utu wa mwanamke na kumpa mtoto wa kike nafasi sawa katika fursa mbalimbali.

“Changamoto ya ndoa za utotoni, mimba za utotoni na mila potofu zinazokwamisha maendeleo ya mwanamke, ikiwamo umiliki wa ardhi, serikali imeendelea kuzishughulikia,” amesema.

Amewataka viongozi wa Jukwaa la Uwezeshaji Wanawake Kiuchumi la Halmashauri ya Mji Handeni kuandaa mpango maalum wa kutoa elimu kwa wanawake ili kuwajengea uwezo wa kutumia fursa zilizopo.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Handeni, Maryam Ukwaju, amesema halmashauri imejipanga kuhakikisha wanawake wanashiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi ili kufikia malengo ya Dira 2050.

Amesema hadi mwisho wa Machi 2026 halmashauri inalenga kusajili angalau vikundi 50 vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu katika mfumo wa NEST ili vinufaike na miradi inayotekelezwa katika eneo hilo.

Awali akisoma risala ya wanawake wa halmashauri hiyo, Carin Umwambe, amesema ukosefu wa maji umekuwa ukisababisha wanawake kutumia muda mwingi kutafuta maji badala ya kujishughulisha na shughuli za maendeleo na kuiomba serikali kuharakisha upatikanaji wa huduma hiyo.

Baadhi ya wananchi waliotembelea banda la Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) katika Kliniki maalum ya kutatua kero za wananchi iliyofanyika katika viwanja vya Nyerere Square, jijini Dodoma, wameshauri Wakala kuanza kujenga nyumba za makazi kwa ajili ya kupangishwa kwa watu binafsi kutokana na kuongezeka kwa mahitaji ya nyumba za kupanga katika mkoa huo.

Ushauri huo umetolewa wakati wa kliniki hiyo iliyolenga kusikiliza na kutatua changamoto mbalimbali za wananchi, sambamba na kuonesha miradi iliyotekelezwa ndani ya siku 100 za Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan tangu kuingia madarakani.

Wananchi hao wamesema kuwa pamoja na mahitaji ya nyumba za makazi kwa watumishi wa umma, bado kuna uhitaji mkubwa wa nyumba za kupanga kwa wananchi wa kawaida wanaoishi katika Jiji la Dodoma.

Bi. Saada Salum, mkazi wa Nzuguni Boda, amesema kuwa upatikanaji wa nyumba za kupanga bado ni changamoto kwa wakazi wengi wa Dodoma, hivyo TBA inapaswa kufikiria kupanua huduma zake ili kuwahusisha pia watu binafsi.

“Suala la nyumba za kupanga hapa Dodoma ni changamoto. Watu wengi wanahitaji nyumba za kupanga. TBA mnatakiwa kufikiria sasa kuanza kujenga nyumba na kupangisha watu binafsi ili nao waweze kukaa kwenye nyumba zenu, si watumishi wa serikali pekee yao,” amesema Bi. Salum.

Kwa upande wake, Peter Masule, mkazi wa Nzuguni kwa Masista, ameishukuru TBA kwa kutekeleza mradi wa ujenzi wa nyumba 3,500 katika eneo hilo, akisema kuwa mradi huo umechangia kuimarika kwa hali ya usalama tofauti na ilivyokuwa awali.

Amesema kabla ya mradi huo kulikuwa na matukio mengi ya uhalifu katika eneo hilo, ambapo wahalifu walikuwa wakitumia vichaka vilivyokuwepo kujificha baada ya kufanya wizi.

“Mimi nimekuwa mkazi wa Nzuguni kwa muda mrefu. Kabla ya mradi wa nyumba hizi kulikuwa na matukio mengi ya uhalifu, vibaka walikuwa wakija kujificha kwenye vichaka baada ya kufanya wizi. Lakini sasa matukio hayo yamepungua sana,” amesema Masule.

Wananchi hao pia wameeleza kuwa uwepo wa mradi wa nyumba hizo umechangia kuboresha mandhari na kupendezesha eneo la Nzuguni.

Kupitia kliniki hiyo, TBA pia imepata fursa ya kukutana na wadau na wateja wake, wengi wao wakiwa ni wapangaji wa nyumba zake, ambapo baadhi ya changamoto walizowasilisha zimepatiwa ufumbuzi papo hapo.

Kliniki hiyo ya siku tatu ilianza Jumatano, Machi 4, 2026 na kuhitimishwa Ijumaa, Machi 6, 2026 katika viwanja vya Nyerere Square jijini Dodoma.

Na Munir Shemweta, WANMM MTWARA

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Leonard Akwilapoamesema jumla ya wananchi 13,550 wamejitokeza kupata huduma mbalimbali za sekta ya ardhi kupitia Samia Ardhi Kliniki iliyofanyika katika mikoa yote 26 nchini.

Dkt. Akwilapo amesema hayo wakati akifunga rasmi Samia Ardhi Kliniki katika viwanja vya Mashujaa mkoani Mtwara tarehe 7 Machi 2026, akisema kliniki hiyo imekuwa jukwaa muhimu la kusogeza huduma za ardhi karibu na wananchi hususan wanawake.

Amesema, kati ya wananchi waliojitokeza katika kliniki hizo, wanawake walikuwa 8,725 sawa na asilimia 64.4 huku wanaume wakiwa 3,892 sawa na asilimia 35.7, jambo linaloonesha mwitikio mkubwa wa wanawake katika kutumia fursa zinazotolewa na Serikali.

Aidha, Waziri Akwilapo amesema, jumla ya hatimiliki 3,131 zimetolewa kwa wananchi waliokamilisha taratibu za umilikishwaji wa ardhi ambapo hatimiliki 2,081 sawa na asilimia 57.4 zimetolewa kwa wanawake na hatimiliki 1,543 sawa na asilimia 43.6 zimetolewa kwa wanaume.

Amefafanua kuwa, hatua hiyo imeongeza usalama wa milki kwa wananchi pamoja na kuimarisha uchumi wa familia na Taifa kwa ujumla.

“Ardhi ni msingi wa uchumi wa mwananchi na Taifa. Mwanamke anapomiliki ardhi kisheria anapata uwezo mkubwa wa kuwekeza, kufanya shughuli za uzalishaji na hata kupata mikopo katika taasisi za fedha,” alisema.

Mkuu wa mkoa wa Mtwara Kanali Donald Msengi amesema, Samia Ardhi Kliniki imenufaisha wanawake kwa kuwaelimisha jambo alilolieza kuwa limelenga kuwawezesha na kulinda haki na kutatua changamoto zao.

‘’Kupitia Kliniki hiyo wanawake walipewa huduma mbalimbali ambazo ni elimu ya kumiliki ardhi, ushauri wa kitaalamu kuhusu masuala ya ardhi pamoja na utoaji hati’’ amesema Kanali Msengi.

Katika hatua nyingine, Dkt Akwilapo amesema, kupitia Samia Ardhi Kliniki jumla ya kero, malalamiko na migogoro ya ardhi 707 zimesikilizwa na kupatiwa ufumbuzi, huku Serikali ikikusanya kiasi cha shilingi milioni 972.16 kupitia huduma mbalimbali zilizotolewa katika kliniki hizo.

Amempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuweka mazingira bora yanayolinda haki za wanawake kupitia maboresho ya sera na sheria mbalimbali zinazolenga kuwawezesha wanawake kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

Amesema, kupitia maboresho ya Sera ya Taifa ya Ardhi ya mwaka 1995 (toleo la mwaka 2023) pamoja na Sheria ya Ardhi na Sheria ya Ardhi ya Vijiji, wanawake wameendelea kutambuliwa kisheria kumiliki, kutumia na kufanya miamala ya ardhi kwa usawa na wanaume.

Waziri Akwilapo pia amewashukuru wadau mbalimbali walioshiriki kufanikisha kliniki hiyo wakiwemo Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Chama cha Wanasheria Wanawake (TAWLA) na Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora kwa kushirikiana na Serikali katika kutoa elimu na msaada wa kisheria kwa wananchi.

Ameongeza kuwa, Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi itaendelea kuendesha kliniki za ardhi katika maeneo mbalimbali nchini ili kurahisisha upatikanaji wa huduma kwa wananchi.

Samia Ardhi Kliniki ilianza Machi 2, 2026 na kuhitimishwa tarehe 7 Machi 2026 ikiwa ni kuelekea kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani ambapo Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi imeanzisha kliniki hiyo kwa lengo kuwafikia wanawake na kuwapatia elimu ya masuala ya ardhi.

Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akizungumza wakati wa kufunga Kliniki Maalum ya Samia Ardhi Kliniki katika viwanja vya Mashujaa mkoani Mtwara tarehe 7 Machi 2026.
Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akimkabidhi Hati Miliki ya Ardhi kwa mmoja wa wakazi wa Mtwara aliyehudumiwa wakati Samia Ardhi Kliniki katika viwanja vya Mashujaa mkoani Mtwara tarehe 7 Machi 2026.
Mkuu wa mkoa wa Mtwara Kanali Donald Msengi akikabidhi hati kwa mwananchi aliyehudumiwa wakati wa Samia Ardhi Kliniki mkoani Mtwara tarehe 7 Machi 2026.
Mkuu wa wilaya ya Mtwara Abdallah Mwaipaya akikabidhi hati milki ya ardhi wakati wa Samia Ardhi Kliniki mkoani Mtwara.
Sehemu ya Watumishi wa Ofisi ya Kamishna wa Ardhi Msaidizi mkoa wa Mtwara wakiwa katika zoezi la kuhudumia wananchi wakati wa Samia Ardhi Kliniki katika viwanja vya Mashujaa mkoani Mtwara.
Baadhi ya wananchi walioshiriki hafla ya kufunga Samia Ardhi Kliniki katika viwanja vya Mashujaa mkoani Mtwara.

Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo (katikati) pamoja na Mkuu wa mkoa wa Mtwara Kanali Donald Msengi (wa pili kushoto) wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kukabidhi hati milki za ardhi kwa wananchi waliohudumiwa wakati wa Samia Ardhi Kliniki katika viwanja vya Mashujaa mkoani Mtwara tarehe 7 Machi 2026. (PICHA ZOTE NA WIZARA YA ARDHI)

Baadhi ya Wanawake wa Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL) wakiwa na Daktari Bingwa Mbobezi wa Magonjwa ya Moyo kwa Watoto - JKCI, Dk. Naizihijwa Majani (katikati) akipokea msaada huo kwa niaba ya Mkurugenzi wa Kituo hicho.



Baadhi ya Wanawake wa Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL) wakiwa na Daktari Bingwa Mbobezi wa Magonjwa ya Moyo kwa Watoto - JKCI, Dk. Naizihijwa Majani (katikati mwenye miwani) akipokea msaada huo kwa niaba ya Mkurugenzi wa Kituo hicho.

Sehemu ya Wanawake wa Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL) wakikabidhi msaada kwa watoto wenye Matatizo ya Moyo katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) - jijini Dar es Salaam, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani.


Baadhi ya Wanawake wa Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL) wakiwa na Daktari Bingwa Mbobezi wa Magonjwa ya Moyo kwa Watoto - JKCI, Dk. Naizihijwa Majani (katikati) akipokea msaada huo kwa niaba ya Mkurugenzi wa Kituo hicho.



Kulia baadhi ya wauguzi wa  Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) - jijini Dar es Salaam, wakiwapatia maelezo baadhi ya Wanawake wa TTCL waliofika kituoni hapo kutoa misaada ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani.

Sehemu ya Msaada uliotolewa na Wanawake wa Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL) wakiwa katika moja ya wodi za watoto kabla ya kugawa kwa wagonjwa.


Baadhi ya Wanawake wa Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL) wakigawa misaada hiyo kwa wagonjwa wa magonjwa ya Moyo kwa Watoto - JKCI.


Daktari Bingwa Mbobezi wa Magonjwa ya Moyo kwa Watoto - JKCI, Dk. Naizihijwa Majani (kushoto) akizungumza na Wanawake wa Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL), kwa niaba ya Mkurugenzi wa Kituo hicho kabla ya kupokea msaada uliowasilishwa kituoni hapo. Wa pili kulia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Wanawake TTCL, Bi. Mercy Amani pamoja na Ofisa Uhusiano wa TTCL, Bi. Adeline Berchimance.


Baadhi ya Wanawake wa Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL) wakipata huduma bure za uchunguzi wa magonjwa ya moyo JKCI mara baada ya kutoa msaada katika kituo hicho.

Na Joachim Mushi, Dar

WANAWAKE wa Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL) leo wametoa msaada kwa watoto wenye Matatizo ya Moyo katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) - jijini Dar es Salaam, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani.

Akikabidhi msaada huo, Mwenyekiti wa Kamati ya Wanawake TTCL, Bi. Mercy Amani alisema wanaungana na taasisi nyingine na makundi mbalimbali kuadhimisha siku ya wanawake kwa kutambua changamoto wanazopata watoto wenye matatizo ya moyo JKCI pamoja na wazazi wao hivyo wameguswa kuwasaidia vitu kadhaa hospitalini hapo.

Alisema miongoni mwa vitu walivyokabidhi ni pamoja na Pampas (diapers), maziwa ya watoto wachanga kwa ajili ya watoto wanaopatiwa matibabu ya moyo hospitalini hapo na taulo za kike kwa ajili ya wazazi na walezi wanaouguza watoto wao katika Taasisi hiyo ya Magonjwa ya Moyo.

"...Kwa niaba ya Wanawake wa TTCL, tumefika hapa katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete kuonesha mshikamano wetu na watoto wenye matatizo ya moyo pamoja na wazazi na walezi wao. Tunatambua kuwa safari ya matibabu hasa ya moyo si rahisi na ndio maana leo tumekuja si tu na msaada wa vifaa, bali pia na ujumbe wa faraja na matumaini," alisema Bi. Mercy Amani akizungumza kwenye hafla hiyo.

" Kipekee tunapenda kuwapongeza na kuwashukuru madaktariwauguzi na wataalamu wote wa afya wa Taasisi hii kwa kazi kubwa ya kujitoa na ya huruma mnayoifanya kila siku kuokoa maisha ya watoto hawa. Huduma zenu ni tumaini kwa familia nyingi na mchango mkubwa kwa taifa letu," alisisiotiza kiongozi huyo wa Wanawake TTCL.

Kwa upande wake, Daktari Bingwa Mbobezi wa Magonjwa ya Moyo kwa Watoto - JKCI, Dk. Naizihijwa Majani akipokea msaada huo kwa niaba ya Mkurugenzi wa Kituo hicho. alisema awali watu wengi walikuwa wakiamini magonjwa ya moyo ni kwa watu wazima tu lakini kwa sasa jamii itambue kuwa watoto wanaugua magonjwa ya moyo na magonjwa haya kwa watoto yapo ya kuzaliwa nayo na yanayokuja baadaye. 

Anabainisha kuwa wengi wa watoto wanaopatiwa matibabu katika kituo hicho ni wale wanaougua magonjwa ya moyo ya kuzaliwa nayo, huku takwimu zikioneshwa kuwa kwa kila watoto 100 wanaozaliwa mtoto mmoja hadi wawili wanazaliwa na tatizo la ugonjwa wa moyo. 

Aidha aliwataka wazazikuwa na utaratibu wa kuwachunguza watoto wao kiafya ili kama watagundulika mapema na matatizo hayo waweze kupatiwa matibabu mapema kabla ya kuathirika zaidi na mashambulizi ya ugonjwa.

Na Munir Shemweta, WANMM MTWARA

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Leonard Akwilapoameshuhudia uapisho wa wajumbe wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya na kuwataka wajumbe hao kutenda haki kuacha kutoa maamuzi ya kuwafurahisha watu wakati wa kusikiliza mashauri ya ardhi.

Uapisho huo umeongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Donald Wilson Msengi, na kufanyika leo tarehe 7 Machi 2026 katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa.

Akizungumza mara baada ya kushuhudia uapisho huo, Dkt. Akwilapo aliwaasa wajumbe wa mabaraza hayo kuepuka kutoa maamuzi kwa lengo la kuwafurahisha watu au makundi fulani, badala yake wafanye maamuzi yanayozingatia haki na sheria ili kupunguza migogoro ya ardhi katika jamii.

Alisema wajumbe wanapaswa kutambua kuwa nafasi waliyopewa ni dhamana kubwa kutoka kwa Mungu na Serikali, hivyo wanatakiwa kuitumia kwa uadilifu, uaminifu na kwa kuzingatia misingi ya haki.

“Napenda mtambue kuwa nafasi mlizopewa ni kwa mapenzi ya Mwenyezi Mungu, hivyo mheshimu Mungu kwa kufanya maamuzi yanayoendana na haki na uadilifu,” alisema Dkt. Akwilapo.

Aliongeza kuwa, kazi ya kushughulikia mashauri ya ardhi si rahisi, kwani mara nyingi huwa na pande mbili zinazopingana, lakini wajumbe wanapaswa kufanya maamuzi kwa kuzingatia ushahidi na sheria ili haki ipatikane kwa anayestahili.

“Sina wasiwasi na ninyi, ingawa kazi ni ngumu, lakini mfanye maamuzi kwa kuzingatia haki na siyo kumfurahisha mtu,” alisisitiza.

Dkt. Akwilapo pia alisema uimarishaji wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya ni sehemu ya jitihada za Serikali za kuimarisha mifumo ya utatuzi wa migogoro ya ardhi kwa kusogeza huduma hizo karibu zaidi na wananchi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Mtwara Kanali Msengi aliwapongeza wajumbe hao kwa kuaminiwa kushika nafasi hizo na kuwataka kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia viapo walivyokula na kufanya kazi kwa weledi.

Amesema, wajumbe wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya ni kiungo muhimu katika mfumo wa utatuzi wa migogoro ya ardhi, hivyo wanapaswa kufanya kazi kwa uadilifu ili kujenga imani kwa wananchi.

“Uwepo wa wajumbe wa mabaraza ya ardhi katika wilaya zenu sasa utawezesha wananchi kupata huduma karibu zaidi badala ya kusafiri umbali mrefu kufuata huduma hizo,” alisema.

Ameongeza kuwa, hatua hiyo itasaidia kupunguza gharama na muda ambao wananchi walikuwa wakitumia kufuata huduma za utatuzi wa migogoro ya ardhi katika maeneo ya mbali.

Wajumbe walioapishwa wanatoka katika wilaya za Mtwara, Tandahimba, Newala pamoja na wilaya ya Nanyumbu mkoani Mtwara.

Serikali kupitia Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi imeendelea kuimarisha Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya wilaya ili kuongeza ufanisi katika kusikiliza na kutatua migogoro ya ardhi kwa wakati, jambo litakalosaidia kuimarisha usalama wa milki na kuleta utulivu katika jamii.

Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akizungumza wakati wa kuapishwa kwa wajumbe wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya mkoani Mtwara tarehe 7 Machi 2026.
Mkuu wa Mkoa wa Mtwara Kanali Donald Msengi akimuapisha mmoja wa wajumbe wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya mkoani Mtwara tarehe 7 Machi 2026.
Baadhi ya maofisa wa idara mbalimbali mkoani Mtwara wakiwa katika hafla ya kuapishwa kwa wajumbe wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya mkoani Mtwara tarehe 7 Machi 2026.
Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo (wa pili kushoto mstari wa mbele) na Mkuu wa mkoa wa Mtwara Kanali Donald Msengi(wa tatu kulia mstari wa mbele) pamoja na viongozi wengine wakiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya mkoani Mtwara walioapishwa tarehe 7 Machi 2026. (PICHA ZOTE NA WIZARA YA ARDHI)

Sehemu ya Wajumbe wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya mkoani Mtwara walioapishwa tarehe 7 Machi 2026
Mkuu wa Mkoa wa Mtwara Kanali Donald Msengi akizungumza wakati wa hafla ya kuwaapisha Wajumbe wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya mkoani Mtwara tarehe 7 Machi 2026

JUMLA  ya wanawake 1916 wamefika katika viwanja vya Ofisi za Ardhi kufuatilia hati zao za ardhi na kupata huduma mbalimbali za masuala ya umiliki wa ardhi kupitia programu maalumu ya Samia Ardhi Kliniki inayofanyika Mkoa wa Dodoma.

Wanawake hao wamejitokeza kwa wingi kupata elimu kuhusu haki za umiliki wa ardhi, ushauri wa kitaalamu pamoja na kusaidiwa kukamilisha taratibu za kupata hatimiliki.

Hayo yamesemwa na Kamishna wa Ardhi Msaidizi Mkoa wa Dodoma Bi.Happiness Mtutwa,wakati akifunga kliniki maalum iitwayo Samia Ardhi Kliniki  yenye Kauli Mbiu, Mwanamke; Haki Yako, Miliki Ardhi sasa.

"Katika kliniki hiyo, huduma mbalimbali zimetolewa ambapo hati 694 zimesajiliwa, hati 316 zimekabidhiwa kwa wanawake, migogoro 49 ya ardhi imetatuliwa, na wanawake 105 wamepata ushauri wa kisheria bila malipo. Mpango huo umeonesha mwitikio mkubwa wa wananchi hususan wanawake katika kufuatilia haki zao za umiliki wa ardhi."amesema Bi.Mtutwa

Amesema kuwa Kliniki hiyo imefanyika kuanzia  Machi 2 hadi 7 Machi 2026, ikiwa ni utekelezaji wa maelekezo ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt. Leonard Akwilapo, aliyoyatoa tarehe 12 Februari 2026 jijini Dodoma wakati akihitimisha Kliniki ya Ardhi. Lengo lake ni kuwapa wanawake fursa ya kupata huduma za ardhi kwa urahisi, sambamba na kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani.

Katika kipindi hicho, viongozi wa mkoa wakiongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Rosemary Senyamule pamoja na Mkuu wa Wilaya Mhe. Jabir Shekimweri walitembelea kliniki hiyo kusikiliza na kutatua changamoto mbalimbali za ardhi zinazowakabili wananchi.

Aidha amesema kuwa Taasisi mbalimbali zilishiriki kutoa huduma za ushauri na msaada wa kisheria, zikiwemo Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Chama cha Wanawake Wanasheria Tanzania (TAWLA), Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, pamoja na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu.

Hata hivyo Bi.Mtutwa amesema kuwa Programu ya Samia Ardhi Kliniki imeendelea kuwa jukwaa muhimu la kuwawezesha wanawake kumiliki ardhi kisheria na kupata haki zao, jambo linalochangia maendeleo ya kiuchumi na kijamii kwa familia na jamii kwa ujumla.

Pia amewataka wanawake hao kwenda kuzitumia vizuri hati hizo ili ziweze kuwasaidia kiuchumi kwa kuweza kwenda nazo benki kwa ajili ya kukopa mikopo nafuu itakayowawezesha kuanzisha biashara na kuendelea kuimarisha uchumi wao.

Sambamba na hilo, Bi.Mtutwa pia amekabidhi hati miliki kwa baadhi ya wanawake waliofika katika kliniki hiyo iliyofanyika katika viwanja vya Ofisi ya Kamishna Msaidizi wa Ardhi Mkoa wa Dodoma.


Top News