Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema kuna umuhimu mkubwa kwa nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki kuimarisha ushirikiano katika nyanja ya diplomasia ya uchumi, biashara na uwekezaji.
Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, tarehe 06 Julai 2026, alipokutana na Balozi mpya wa Tanzania nchini Uganda, Mhe. Balozi Meja Jenerali Marco Elisha Gaguti, aliyefika Ikulu Zanzibar kwa ajili ya kuaga kabla ya kuelekea katika kituo chake cha kazi.
Rais Dkt. Mwinyi amesema ni wakati muafaka kwa nchi za Afrika Mashariki kuendelea kuimarisha ushirikiano wa kibiashara na uwekezaji, kwa lengo la kunufaika na fursa mbalimbali za kiuchumi zilizopo katika mataifa hayo.
Ameeleza kuwa uhusiano mzuri baina ya mataifa hayo ni msingi muhimu wa kukuza uchumi na kuimarisha ustawi wa wananchi.
Aidha, Rais Dkt. Mwinyi amemsisitiza Balozi Marco kutumia nafasi yake kuzitangaza fursa za uwekezaji na vivutio vya utalii vilivyopo Tanzania, ikiwemo Zanzibar, nchini Uganda, hususan kwa makampuni, wafanyabiashara na wawekezaji wakubwa, ili waweze kuja kuwekeza nchini.
Rais Dkt. Mwinyi amemhakikishia Balozi Marco ushirikiano mkubwa katika utekelezaji wa majukumu yake mapya ya kibalozi, huku akimshauri kuchukua juhudi maalum za kuwashawishi na kuwaunganisha wafanyabiashara na wawekezaji wa Uganda kutumia fursa zilizopo kuwekeza Tanzania.
Kwa upande wake, Mhe. Balozi Meja Jenerali Marco Elisha Gaguti amemhakikishia Rais Dkt. Mwinyi kuwa atafanya kila linalowezekana kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi, kwa kuzingatia miongozo na maelekezo aliyopokea, sambamba na kuendeleza kimkakati diplomasia ya uchumi baina ya Tanzania na Uganda.
Benki ya NMB imesema huduma ya NMB Kikundi Mini App, iliyopo ndani ya NMB Mkononi Super App, imebuniwa kurahisisha usimamizi wa vikundi kwa kuwawezesha wanachama na viongozi kupata huduma za kifedha kidigitali kwa usalama, uwazi na ufanisi zaidi.
Akizungumza katika Banda la NMB kwenye Maonesho ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam, maarufu Sabasaba, Meneja wa Kanda, Huduma za Vikundi na Benki Vijijini wa NMB, Dismas Prosper, alisema mfumo huo unapunguza muda na gharama za kupata huduma za benki, huku ukiimarisha usalama wa miamala na kurahisisha shughuli za vikundi mbalimbali vya kijamii na kiuchumi.
Prosper alisema kupitia NMB Kikundi Mini App, wanachama wa vikundi wanaweza kufungua akaunti bila kutembelea tawi la benki, kufanya miamala kwenda benki nyingine na mitandao ya simu, pamoja na kuweka michango yao moja kwa moja kwenye akaunti ya kikundi. Aidha, alisema kila mwanachama hupokea ujumbe mfupi wa simu unaothibitisha mchango uliowekwa, hatua inayoongeza uwazi na uwajibikaji katika usimamizi wa fedha za kikundi.
Aliongeza kuwa mfumo huo pia unawawezesha wanachama kuona taarifa za hisa, idadi na majina ya wanachama wa kikundi, pamoja na taarifa binafsi za kila mwanachama kulingana na mamlaka aliyopewa ndani ya mfumo. Prosper alisema ubunifu huo ni sehemu ya jitihada za NMB kuendelea kuleta suluhisho za kidigitali zinazowawezesha wananchi, hususan vikundi vya kijamii na kiuchumi, kupata huduma za kifedha kwa urahisi, usalama na uwazi zaidi.

Na Oscar Assenga,TANGA
Wazazi, walezi na waajiri nchini wamehimizwa kuhakikisha watoto wanawakatia bima ya afya mapema ili kuwaepusha na changamoto za gharama kubwa za matibabu na kuwawezesha kupata huduma za afya kwa wakati wanapougua.
Wito huo umetolewa leo na Afisa Matekelezo wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) Mkoa wa Tanga, Macrina Clemens, wakati wa utoaji wa elimu kuhusu bima ya afya ulioambatana na zoezi la upimaji wa afya na usajili wa wanachama wa vifurushi mbalimbali katika Kanisa la KKKT Ushirika wa Makorora, jijini Tanga.
.jpg)
Akizungumza na waumini wa kanisa hilo, Macrina alisema afya ni mtaji muhimu kwa maendeleo ya familia na Taifa, hivyo kujiunga na bima ya afya ni uwekezaji unaowalinda wananchi dhidi ya gharama zisizotarajiwa za matibabu.
Alisema wazazi wanaowakatia watoto wao bima ya afya hupata uhakika wa matibabu wakati wowote mtoto anapougua, jambo linalowapa utulivu wa akili na kuwawezesha watoto kuendelea na masomo bila kukatishwa na changamoto za kifedha.
.jpg)
“Mzazi anapokuwa na bima ya afya kwa mtoto wake anakuwa na uhakika wa kupata matibabu kwa wakati, hivyo kuepuka usumbufu wa kutafuta fedha za dharura kila ugonjwa unapojitokeza,” alisema.
Macrina alisema wanafunzi wanaosoma katika shule mbalimbali wanaweza kujiunga na bima ya afya kupitia shule zao kwa gharama ya Sh50,400 kwa mwaka mzima wa masomo, huku watoto ambao bado hawajaanza shule wakijiunga kupitia vifurushi mbalimbali vinavyotolewa na NHIF.

Alisema Serikali inaendelea kutekeleza azma ya kuhakikisha kila Mtanzania anakuwa na bima ya afya, hivyo akazitaka taasisi za elimu, wazazi, walezi, waajiri na wamiliki wa kampuni binafsi kutumia fursa hiyo kuwaandikisha watoto na wafanyakazi wao.
“Bima ya afya si gharama, ni kinga ya maisha. Ukiwa na bima unakuwa na uhakika wa kupata daktari, dawa na huduma za matibabu bila kubeba mzigo mkubwa wa kifedha pale unapougua,” alisema.

NHIF imeendelea kutoa elimu kwa makundi mbalimbali ya wananchi kuhusu umuhimu wa bima ya afya ikiwa ni sehemu ya juhudi za Serikali za kuongeza idadi ya Watanzania wanaonufaika na huduma hiyo na kuimarisha upatikanaji wa huduma bora za afya nchini.



Waziri wa Afya wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mohamed Mchengerwa ametoa mwito wa mashirikiano ya kisayansi katika utafiti ugonjwa wa kifua kikuu baina ya Tanzania na China ili kuutibu ugonjwa huo katika kipindi kifupi tofauti na hali ilivyo sasa.
Mchengerwa ametoa mwito huo leo katika Kituo cha Shanghai Sci-Tech Inno Center for Infection & Immunity kilichopo Shanghai, nchini China akipendekeza ushirikiano wa kimkakati kati ya Tanzania na China unaolenga utafiti wa kifua kikuu (TB), ubunifu wa kitabibu, na maendeleo ya dawa.
Katika hotuba yake, mbele ya wanasayansi wabobezi wa utafiti akiwemo Mkurugenzi Dkt. Zhang Wenhong, pamoja na wawakilishi wa Chuo Kikuu cha Fudan na Hospitali Maarufu ya Huashan ya nchinib China, amesisitiza umuhimu wa ushirikiano wa kimataifa katika sayansi ya magonjwa ya kuambukiza.
Waziri Mchengerwa ambaye ameongoza Timu ya wataalam kutoka Tanzania na Naibu Katibu Mkuu anayeshughulikia Dawa na vifaaa tiba Emmanuel Tayari ametembelea maabara ya kituo hicho na kijionea vifaa vya kisasa vya uchunguzi wa magonjwa mbalimbali.
Waziri amekipongeza Kituo cha Shanghai Sci-Tech Inno Center for Infection & Immunity kuwa miongoni mwa vitovu kinachoongoza duniani ambapo utafiti wa kisasa kuhusu maambukizi, kinga ya mwili, na usalama wa kibaiolojia unatafsiriwa kuwa matokeo halisi ya kitabibu.
Amependekeza kuanzisha ushirikiano rasmi kati ya kituo hicho cha Shanghai na Hospitali ya Kibong'oto ambayo ameielezea kuwa ni taasisi ya kihistoria inayojihusisha na matibabu na utafiti wa kifua kikuu nchini Tanzania kwa mafanikio makubwa.
Aidha, Waziri Mchengerwa amesisitiza kuwa kila taasisi ina nguvu zake za kipekee: Shanghai ina uwezo mkubwa katika genomiki, kinga ya mwili (immunology), uchunguzi wa magonjwa, na sayansi ya kompyuta, wakati Kibong'oto inatoa uzoefu wa karibu karne moja wa kliniki katika udhibiti wa TB, ikiwa ni pamoja na nyaraka adimu za kihistoria za wagonjwa zinazoanzia mwaka 1926.
"Hospitali ya Kibong'oto liyopo katika miteremko ya Mlima Kilimanjaro katika Mkoa wa Kilimanjaro ilianzishwa mwaka 1926 kama sanatorium ya kifua kikuu. Baada ya muda, ilibadilika kutoka kituo cha matibabu hadi hospitali ya rufaa ya kitaifa ya kisasa, na tangu 2006 imekuwa kituo cha kitaifa cha Tanzania cha kifua kikuu sugu". Amefafanua Mhe. Mchengerwa
Amependekeza hospitali ya Kibong'oto kuweka nyaraka zake yenye zaidi ya miaka 100 katika mfumo wa kidijitali na kuzichambua kisayansi ili kufungua njia mpya za kuelewa usugu wa dawa na mabadiliko ya magonjwa, hasa zikichanganywa na zana za kisasa za matibabu ya ugonjwa huo zinazopatikana katika Kituo cha Shanghai.
Ameyataja baadhi ya maeneo muhimu ya ushirikiano kuwa ni pamoja na Utafiti wa TB sugu ya dawa, unaolenga epidemiolojia ya molekuli na uchunguzi wa haraka unaofaa mazingira halisi ya kliniki.
Mabadilishano ya kitaaluma na kitabibu, kuruhusu wataalamu wa Tanzania na China kujifunza katika taasisi za kila upande
Uwekaji kidijitali wa nyaraka za kihistoria za Kibong'oto, kubadilisha data ya miongo mingi kuwa rasilimali ya kisasa ya utafiti na
Kuimarisha mifumo ya maabara na ufuatiliaji nchini Tanzania, kusaidia ufuatiliaji wa ugonjwa huo.Pia Waziri Mchengerwa ameeleza kuwa dhamira ya Serikali ya Tanzania ni kuhama kutoka kuagiza dawa hadi kuzalisha ndani ya nchi.
Alialika ushirikiano na washirika wa China kusaidia uzalishaji wa ndani wa dawa za TB, vifaa vya uchunguzi, na huenda hata chanjo za baadaye ambapo ingejumuisha uhamishaji wa teknolojia, mafunzo ya wataalamu, na ujenzi wa mifumo ya ubora wa uzalishaji ndani ya Tanzania.
" Hili si tu lengo la kiuchumi, bali ni suala la uhuru wa kisayansi na ustahimilivu wa muda mrefu wa afya ya umma". Amesisitiza Mchengerwa
Pia amesisitiza kuwa miundombinu itakayojengwa kupitia ushirikiano huu inaweza kuwa msingi wa kukabiliana na magonjwa mapya ya milipuko katika siku zijazo ambapo amesema mchanganyiko wa uzoefu wa kliniki wa Tanzania na uwezo wa utafiti wa China utaimarisha maandalizi ya kimataifa dhidi ya magonjwa yanayoibuka.
Akihitimisha hotuba, Waziri alisisitiza tena dhamira ya Tanzania ya kushirikiana badala ya kutegemea misaada, akisisitiza uwekezaji katika taasisi za kitaifa na uwezo wa kisayansi.
Alitoa mwito wa moja kwa moja kwa Mkurugenzi Zhang na wenzake Shanghai kuhamia kutoka majadiliano kwenda makubaliano rasmi na utekelezaji—akiona ushirikiano huo kama daraja la muda mrefu kati ya uzoefu wa kitabibu Afrika Mashariki na ubunifu wa kibayomedisini China.
"Iwapo utatekelezwa, mpango huu unaweza kuwa mfano adimu wa ushirikiano wa usawa katika afya ya kimataifa—ukiunganisha uzoefu wa muda mrefu wa kliniki na sayansi ya kisasa katika juhudi ya pamoja ya hatimaye kuishinda kifua kikuu". Amefafanua Mchengerwa.
Na Mwandishi Wetu
BODI ya Utalii Tanzania (TTB) imemkabidhi rasmi mwanautalii na mtangazaji wa vivutio vya utalii kutoka Oman, Khalid Hamed Al Barwani, Ubalozi wa Hiari wa Utalii wa Tanzania, ikiwa ni hatua ya kimkakati ya kuimarisha juhudi za kuitangaza Tanzania katika masoko ya kimataifa na kuongeza idadi ya watalii wanaotembelea nchini.
Ubalozi huo umekabidhiwa na Mkurugenzi Mkuu wa TTB, Ephraim Mafuru, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, ikiwa ni kutambua mchango mkubwa wa Al Barwani katika kuitangaza Tanzania kupitia majukwaa mbalimbali ya kimataifa.
Al Barwani alipata umaarufu mkubwa baada ya kuongoza kundi la Dream Team Explorers kutembelea Shamba la Miti la Sao Hill mwaka 2024, ambapo walijionea vivutio vya kipekee vinavyopatikana katika eneo hilo, ikiwemo misitu ya kupandwa, mandhari ya kuvutia ya asili na eneo la Mto Ruaha.
Maudhui waliyoyashiriki kupitia majukwaa yao ya kidijitali yalichangia kuongeza mwonekano wa Sao Hill na kuibua hamasa ya watalii wa ndani na nje ya nchi kutembelea eneo hilo.
Akizungumza wakati wa hafla ya kukabidhi ubalozi huo, Mafuru alisema TTB itaendelea kushirikiana na watu mashuhuri, watengeneza maudhui na wadau wa kimataifa wenye ushawishi mkubwa katika masoko mbalimbali ili kuendelea kuitangaza Tanzania kama moja ya vivutio bora vya utalii duniani.
“Ubalozi huu ni kutambua mchango wa Khalid Al Barwani katika kuitangaza Tanzania na ni sehemu ya mkakati wetu wa kupanua wigo wa masoko ya utalii kupitia mabalozi wa hiari wanaotumia ushawishi wao kufikisha ujumbe wa Tanzania kwa mamilioni ya watu duniani,” alisema Mafuru.
Kwa upande wake, Al Barwani alishukuru kwa heshima hiyo na kuahidi kuendelea kuitangaza Tanzania kupitia majukwaa yake ya kimataifa, akieleza kuwa nchi ina vivutio vya kipekee vinavyostahili kufahamika zaidi duniani.
“Tanzania ni nchi yenye uzuri wa kipekee, kuanzia hifadhi za wanyamapori, misitu, fukwe, utamaduni hadi ukarimu wa wananchi wake. Nitaendelea kuwa balozi wa kuitangaza Tanzania kwa dunia,” alisema.
TTB inaendelea kutumia ushirikiano na wadau wa kimataifa pamoja na mabalozi wa hiari wa utalii kama sehemu ya mkakati wa kuongeza ushindani wa Tanzania katika soko la utalii duniani na kuunga mkono malengo ya taifa ya kukuza sekta ya utalii, kuongeza idadi ya wageni wa kimataifa na kuongeza mchango wa sekta hiyo katika maendeleo ya uchumi wa nchi.

-Wasema unaongeza uwazi, ufanisi na kuokoa muda wa kupata huduma
Na Grace Michael, Dar es Salaam
WANANCHI na wanachama wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) wamepongeza Mfumo wa Kujihudumia Binafsi (Self Service) unaowezesha wanachama kupata huduma mbalimbali kupitia simu janja, wakisema mfumo huo umeongeza uwazi katika utoaji wa huduma, kurahisisha upatikanaji wa taarifa na kuokoa muda ambao awali walilazimika kuutumia kufika katika ofisi za NHIF.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti walipotembelea banda la NHIF katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, wananchi hao walisema maboresho ya mifumo ya kidijitali ya NHIF yameongeza ufanisi na kuimarisha usimamizi wa huduma za bima ya afya.
Bw. Emmanuel Selemani alisema mfumo huo unampa mwanachama uwezo wa kuona historia ya huduma zote alizopata katika vituo vya kutolea huduma za afya, hatua inayochangia kuongeza uwazi na kuwapa wanachama nafasi ya kushiriki katika kulinda rasilimali za Mfuko.
"Mfumo huu ni mzuri sana kwa sababu kila mwanachama anaweza kuona huduma alizopata katika kituo cha afya. Ikitokea kuna huduma zimeonekana kwenye mfumo lakini hakuzipata, anaweza kutoa taarifa NHIF ili zifuatiliwe. Hii itasaidia kudhibiti na kuzuia vitendo vya udanganyifu katika utoaji wa huduma," alisema.
Kwa upande wake, Bi. Maria Nzalima alisema ameridhishwa na huduma zinazotolewa katika banda la NHIF kwenye maonesho hayo kutokana na kasi ya utoaji wa huduma pamoja na elimu aliyopata kuhusu haki na wajibu wa mwanachama wa NHIF.
"Huduma ni za haraka na nimepata elimu muhimu kuhusu namna ya kutumia bima yangu pamoja na haki na wajibu wangu kama mwanachama. Hii imeniongezea uelewa na kujiamini ninapotumia huduma za NHIF," alisema.
Akizungumza kuhusu huduma zinazotolewa katika banda la NHIF, Ofisa Uanachama Mwandamizi, Bw. Hassan Ally, alisema wananchi wanapata huduma mbalimbali ikiwemo usajili kupitia vifurushi mbalimbali vya bima ya afya, elimu ya matumizi ya Mfumo wa Self Service, uhuishaji wa taarifa za wanachama, kubadilisha namba za simu pamoja na kuunganisha taarifa zao na Mfumo wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA).
Aliongeza kuwa maonesho hayo yanatoa fursa muhimu kwa wananchi kupata elimu kuhusu huduma za NHIF na kujisajili ili waweze kunufaika na huduma za bima ya afya.
"Tunawahamasisha wananchi wote kutembelea banda la NHIF lililopo ndani ya Banda la Kijiji cha Bima ili kupata elimu, kujisajili na kufahamu huduma mbalimbali zinazotolewa na Mfuko kwa wanachama wake," alisema.
NHIF imeendelea kushiriki Maonesho ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam kila mwaka ikiwa ni sehemu ya jitihada za kusogeza huduma kwa wananchi, kutoa elimu kuhusu bima ya afya na kuhamasisha ushiriki katika utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote. ”Bima ya Afya kwa Wote, Jiunge Sasa."
.jpeg)








.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)



.jpeg)
.jpeg)



.jpeg)
.jpeg)




.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)



.jpeg)


.jpeg)