Wakala ya Barabara Tanzania (TANROADS) umebaini kuwepo kwa watu wanaojihusisha na vitendo vya utapeli kwa kujifanya watumishi wa wakala, maeneo mbalimbali hususani katika mkoa wa Dodoma.

Kwa mujibu wa taarifa kwa umma iliyotolewa na Mtendaji Mkuu wa TANROADS mapema wiki hii, imeelezwa kuwa taarifa zilizopokelewa zinaonyesha matapeli hao wamekuwa wakiwasiliana kwa njia ya simu na wamiliki wa mabango ya matangazo (billboards), nakujitambulisha kama maafisa wa TANROADS na kudai malipo ili kuzuia kuondolewa kwa mabango yaliyokwisha muda wake.

Taarifa hiyo imeongeza kuwa mbinu zinazotumika na matapeli hao ni pamoja na kutumia lugha ya mamlaka, kutoa vitisho vya kuchukua hatua za kisheria, na kuwaharakisha walengwa kufanya malipo ili kuepuka hatua hizo. Hali hii imekuwa ikiwalenga zaidi wafanyabiashara na wamiliki wa mabango ambao mikataba yao imefikia ukomo.

Kutokana na udanganyifu huo, baadhi ya wananchi tayari wameathirika kwa kupoteza fedha zao baada ya kutuma malipo kwa namba binafsi walizopewa na matapeli hao. TANROADS imesisitiza kuwa haitoi huduma kwa kupokea malipo kupitia namba binafsi za simu au kwa mtu mmoja mmoja, Badala yake, malipo yote hufanyika kupitia mifumo rasmi ya serikali inayotambulika.

Wananchi wametahadharishwa kuwa makini, kuthibitisha taarifa kabla ya kufanya malipo yoyote, na kuepuka kabisa kutuma fedha kwa mtu yeyote anayewasiliana kwa njia hiyo na kujitambulisha kama mtumishi wa TANROADS bila kufuata taratibu rasmi.

Ameeleza kuwa, TANROADS inaendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi kufuatilia utapeli huo ili kuwabaini wahusika na kuchukua hatua kali za kisheria dhidi yao

Wananchi wote wamehimizwa kutoa taarifa za matukio ya aina hiyo kupitia ofisi za TANROADS zilizo karibu au kwa kutumia njia rasmi za mawasiliano za wakala huo, Ushirikiano wa wananchi unatajwa kuwa muhimu katika kusaidia kukomesha vitendo hivyo vya uhalifu.

TANROADS imeeleza kuwa itaendelea kuchukua hatua madhubuti kulinda maslahi ya wananchi na kuhakikisha huduma zake zinatolewa kwa uwazi, usalama na uadilifu, huku ikiwataka wananchi kuwa sehemu ya mapambano dhidi ya matapeli kwa kutoa taarifa mapema wanapobaini viashiria vya udanganyifu.



WIZARA ya Kilimo imesema mafanikio katika kilimo cha mpunga nchini yametokana na uwekezaji wa kimkakati wa Serikali, huku ikiielekeza COPRA kuimarisha usimamizi wa masoko ili kuongeza tija.

Akizungumza katika ufunguzi wa Mkutano wa Kitaifa wa Wadau wa Zao la Mpunga uliofanyika Machi 30, 2026 mkoani Morogoro, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo anayesimamia Maendeleo ya Mazao na Usalama wa Chakula, Prof. Peter L. M. Msofe, alisema sekta hiyo imepata mageuzi makubwa.

Alisema uzalishaji wa mchele umefikia tani milioni 2.6 katika mwaka 2024/2025, ukilinganishwa na mahitaji ya tani milioni 1.2, hali iliyoifanya Tanzania kuwa na ziada ya tani milioni 1.4.

Prof. Msofe aliongeza kuwa ziada hiyo imewezesha kuuza nje tani 298,715 za mchele katika masoko ya EAC na SADC na kuingiza zaidi ya shilingi bilioni 333.5 za fedha za kigeni.

Pamoja na mafanikio hayo, alibainisha kuwa bado kuna fursa ya kuongeza tija zaidi, akieleza kuwa wastani wa uzalishaji ni tani 3.2 kwa hekta dhidi ya uwezo wa kufikia tani 6 kwa hekta.

Aidha, alisema Serikali inalenga kuongeza uzalishaji hadi tani milioni 8 ifikapo 2030 na kupunguza upotevu wa mazao baada ya mavuno kutoka asilimia 25 hadi chini ya asilimia 10.

Kwa upande wa COPRA, Bi. Pendo Biganmbo, Mkurugenzi wa Idara ya Maendeleo ya Mazao na Viwango, aliyemwakilisha Mkurugenzi Mkuu, alisema wameanza usajili na utoaji wa leseni kwa wafanyabiashara wa mpunga ili kuimarisha usimamizi wa soko.

Alisema zoezi hilo litahusisha pia wakulima kusajiliwa pamoja na mashamba yao ili kuongeza ufanisi katika mnyororo mzima wa thamani wa zao la mpunga.
Shirika la Utafiti na Maendeleo ya Viwanda Tanzania (TIRDO) imewaalika wadau wa ngozi nchini kupata mafunzo juu ya uchakataji na utengenezaji bidhaa za ngozi nchini .

Hayo yameelezwa na Kaimu Mkurugenzi wa TIRDO Mhandisi Ramson Mwilangali wakati akifunga mafunzo ya siku tano kwa wanafunzi na wazalishaji wa Bidhaa za ngozi nchini .

Mafunzo hayo ya siku tano yamelenga kuwajengea uwezo wazalishaji wa ngozi kutoka mikoa ya Pwani , Morogoro,Dar es salaam na Kilimanjaro lengo likiwa ni kuhakikisha ngozi inayozalishwa hapa nchini inachakatwa na kuzalisha bidhaa tofauti na sasa ambapo kwa kiasi kikubwa ngozi inauzwa nje ya nchi kabla ya kuchakatwa .

Mhandisi Ramso amesema kuwa soko la Tanzania inahitaji zaidi ya jozi ya viatu milioni 54 huku Viwanda vya ndani vikizalisha jozi elfu tatu tu ambayo ni chini ya asilimia kumi ya mahitaji bidhaa hiyo kwa mwaka.

"Tunalenga kuongeza uzalishaji wa ndani kufikia asilimia 50 ya mahitaji ya nchi ili kuziba pengo linaloagizwa kutoka nje .

Kwa upande wa mtaalam ngozi wa na nguo kutoka TIRDO Mhandisi Yusufu Sampuli amesema kuwa lengo lilikuwa ni kutoka mafunzo kwa watu 15 lakini kutokana na uhitaji wamefika watu 28 kutoka mikoa hiyo mitano . "Tumepokea wanufaika wa mafunzo haya waliopo katika hatua mbali mbali ,wengine wamewahi kuzalisha viatu ,wengine ni mara yao ya kwanza lakini Kila Mmoja ametoka hapa na utaalam wa kutosha juu ya hatua za uzalishaji na utambuzi wa ubora wa ngozi aliongeza Mhandisi Sampuli.

Mafunzo hayo yametoleaa kwa wazalishaji wa bidhaa kama viatu, mabegi ,mikanda nk kwa wamiliki wa viwanda vidogo pamoja na wajasiriamali wadogo na wakubwa juu ya elimu ya uboreshaji bidhaa za ngozi.

Baadhi ya wanufaika wa mafunzo hayo Bi.Yusra Omary Ally Kutoka Dar es salaam , Ndugu Piscus Maresh kutoka Pwani na Bi Pauline Kawa wameshukuru Kwa mafunzo hayo na kuishukuru TIRDO Kwa kuwapa nafasi ya kujifunza.

Mmoja wa washiriki hao Bi Yusra Omary amesema kuwa ni mara yake ya kwanza kupata mafunzo hayo lakini ndani ya siku nne ameweza kutengeneza kiatu kwa hatua ya kwanza ya kupima ngozi, kukata hadi kukamilika kabisa. "Mimi siku zote nilikuwa na wazo lakini sikujua nianzie wapi ,kupitia mafunzo haya Sasa naweza kutengeneza kiatu katika hatua zote aliongeza Bi Yusra.

Mafunzo hayo yamedhaminiwa na Wizara ya Viwanda na Biashara , Jumuhia ya Umoja wa Ulaya ,Jumuhia ya Afrika Mashariki pamoja na kituo Cha Biashara cha Kimataifa (ITC ) chini ya mradi wake wa MARKUP II inayolenga kusaidia uzalishaji wa Bidhaa Bora za ngozi barani Afrika .

Wataalam kutoka TIRDO walioshiriki katika kufanikisha mafunzo hayo kwa vitendo Mhandisi Yusufu Sampuli, Kenan Tarimo , Paul Kimathi pamoja na Innocent Barongo ambao kwa pamoja wametoa wito kwa wanufaika hao wa mafunzo kutosita kuwasiliana nao pamoja na kufika TIRDO kupata ushauri wa kitaalam pamoja na upimaji wa Kimaabara.












Jumla ya washiriki 37 kutoka Mamlaka ya Usafiri wa Anga ya Uganda(UCAA), Mamlaka ya Usafiri wa Anga ya Somalia(SCAA) na nchi za Sierra Leone, Liberia na Guinea (Conakry), ambazo zinajumuishwa katika Roberts Flight Information Region (Roberts FIR), wamehitimu mafunzo kozi nne tofauti yaliyolenga kuimarisha usalama na ufanisi wa sekta ya usafiri wa anga barani Afrika katika Chuo cha Usafiri wa Anga (CATC).
 
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) Bw. Salim Msangi, amefunga rasmi kozi hizo za Usimamizi wa Uongozaji Ndege katika hafla iliyofanyika Aprili 2, 2026 katika Makao Makuu ya TCAA, Ukonga–Banana, Dar es Salaam.

Akizungumza, katika hafla hiyo Bw. Msangi aliwapongeza wahitimu kwa juhudi, nidhamu na mafanikio waliyoonesha, na kutoa shukrani kwa mamlaka za anga za Somalia, Uganda, na Robert FIR kwa kushirikiana na CATC katika kuendeleza taaluma ya usafiri wa anga.

Bw. Msangi alisisitiza umuhimu wa Tanzania kuendelea kuwa kitovu cha mafunzo ya usafiri wa anga barani Afrika kutokana na uwekezaji katika miundombinu ya mafunzo na mazingira rafiki ya kujifunzia.

Bw. Msangi pia aliwahimiza wahitimu kufuata taratibu za usalama, kufanya kazi kwa umakini, kudumisha mawasiliano sahihi, na kuweka usalama mbele katika utekelezaji wa majukumu yao.

Kwa upande wake Mkuu wa chuo cha CATC, Bw. Aristid Kanje, alisema kuwa mafunzo haya yamejwajengea washiriki uwezo wa kitaaluma kwa wahitimu na kuwawezesha kutoa huduma ya udhibiti wa anga kwa usalama, kwa ufanisi na kwa weledi.

Mchanganuo wa kozi zilizohitimishwa ni pamoja na kozi ya ‘Basic Aerodrome Control’, iliyohusisha washiriki 21 kutoka SCAA, iliyoanza tarehe 13 Oktoba hadi 21 Novemba 2025; kozi ya ‘Aerodrome Control’, iliyohusisha washiriki 21 kutoka SCAA, iliyoanza tarehe 24 Novemba 2025 hadi 30 Januari 2026; kozi ya ‘Area Control Procedural’, iliyohusisha washiriki 21 kutoka SCAA, iliyoanza tarehe 2 Februari hadi 3 Aprili 2026; pamoja na kozi ya ‘Basic Aerodrome’, iliyohusisha washiriki 16 kutoka Mamlaka ya Usafiri wa Anga ya Uganda (UCAA) na Roberts FIR, iliyoanza tarehe 23 Februari hadi 3 Aprili 2026.

Aidha, Bw. Ahemed Moulin Hasson kutoka SCAA alitoa shukrani na kuhimiza mshikamano kati ya mamlaka za anga za Afrika na CATC, akisisitiza umuhimu wa kushirikiana katika kuimarisha usalama na ufanisi wa anga.

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) Salim Msangi akizungumza na wahitimu wa kozi mbalimbali wakati wa kufunga kozi hizo zilizokuwa zinatolewa na CATC.


Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Somalia (SCAA) Ahemed Moulin Hasson akizungumza namna Mamlaka hiyo inavyotoa nafasi kwa watumishi wao kusoma kozi mbalimbali.

Mkuu wa Chuo cha Usafiri wa Anga (CATC), Aristid Kanje akizungumza kuhusu Chuo hicho kilivyoweza kutoa mafunzo ambayo yamewajengea uwezo wa kitaaluma kwa wahitimu ili kuwawezesha kutoa huduma ya udhibiti wa anga kwa usalama, kwa ufanisi na kwa weledi.










Baadhi ya wahitimu, walimu pamoja na watumishi kutoka CATC, SCAA na TCAA wakifuatilia hotuba ya mgeni rasmi Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) Salim Msangi alipokuwa anafunga kozi hizo.





Mgeni rasmi Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) Salim Msangi pamoja Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Somalia (SCAA) Ahemed Moulin Hasson wakikabidhi vyeti kwa wahitimu.




Mgeni rasmi Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) Salim Msangi pamoja Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Somalia (SCAA) Ahemed Moulin Hasson wakiwa kwenye picha ya pamoja na baadhi ya wahitimu, Baadhi ya Menejimenti ya TCAA na walimu wa CATC wakati wa kufunga kozi hizo

Morogoro

Bodi ya Tano ya Ushauri ya Wizara kwa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) imeanza rasmi majukumu yake kwa kufanya kikao cha 47 cha Bodi, ambacho pia ni kikao cha kwanza cha bodi hiyo mpya.

Kikao hicho kimefunguliwa leo Aprili 2, 2026 mkoani Morogoro na Mwenyekiti wa Bodi hiyo, Luteni Mstaafu Chiku Abdallah Sumbu Gallawa, katika Ukumbi wa Kituo cha Mbegu Bora za Miche ya Miti cha TFS.

Kabla ya kikao hicho, wajumbe walifanya vikao vya kamati kuanzia Machi 31 hadi Aprili 1, 2026, kujadili masuala mbalimbali ya kiutendaji ya wakala.

Pamoja na mambo mengine, Bodi ilipokea na kujadili Mpango wa Biashara wa TFS kwa mwaka wa fedha 2026/2027, sambamba na taarifa mbalimbali za utekelezaji wa majukumu ya taasisi.

Kuanza kwa kikao hicho kunafuatia uzinduzi wa Bodi hiyo uliofanywa Februari 13, 2026 jijini Dodoma na Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Ashatu Kijaji.












Benki Kuu ya Tanzania (BoT) imeamua kuendelea kubakiza kiwango chake cha riba ya msingi ya ukopeshaji (benchmark lending rate) katika asilimia 5.75 kwa robo ya pili ya mwaka huu, ikionesha tahadhari kufuatia kuongezeka kwa sintofahamu katika uchumi wa dunia.

Uamuzi huo ulifikiwa katika kikao cha hivi karibuni cha Kamati ya Sera ya Fedha (MPC), ambapo watunga sera walitathmini hatari zinazotokana na mazingira ya kimataifa dhidi ya uimara wa uchumi wa ndani.

Akizungumza kuhusu uamuzi huo, Naibu Gavana wa BoT, Dkt. Yamungu Kayandabila, alisema hatua hiyo inalenga kusawazisha kati ya kukuza uchumi na kudhibiti mfumuko wa bei.

“Haikuwa uamuzi rahisi,” alisema, akieleza kuwa mvutano wa kisiasa unaoendelea katika Mashariki ya Kati umeanza kuathiri mwenendo wa masoko ya dunia.

Alifafanua kuwa mvutano huo umevuruga minyororo ya usambazaji wa bidhaa na kuchangia kupanda kwa bei, hususan mafuta ambayo sasa yamevuka dola za Marekani 100 kwa pipa, juu ya makadirio ya awali.

Katika hatua nyingine, MPC ilitangaza kupunguza wigo wa riba (interest rate corridor) unaozunguka kiwango cha CBR kutoka pointi 200 hadi 150 za msingi (basis points), hatua inayoweka kiwango cha riba ya siku saba kati ya benki katika viwango vya asilimia 4.25 hadi 7.25.

Kwa mujibu wa Dkt. Kayandabila, hatua hiyo inalenga kuongeza ufanisi wa utekelezaji wa sera ya fedha, huku ikidumisha uthabiti wa bei na kusaidia ukuaji wa uchumi.

Licha ya changamoto za kimataifa, BoT imeeleza kuwa uchumi wa ndani unaendelea kuonesha uimara.

Katika robo ya kwanza ya mwaka, uchumi ulikua kwa asilimia 6.2 Tanzania Bara na asilimia 6.7 Zanzibar, ukichochewa na sekta za ujenzi, kilimo, utalii na huduma za kifedha.

Kwa robo ya pili, ukuaji unatarajiwa kufikia asilimia 6.1 kwa Tanzania Bara na asilimia 6.6 Zanzibar, ingawa hatari za nje zinaweza kuathiri mwenendo huo endapo zitaongezeka.

Kwa upande wa mfumuko wa bei, umeendelea kubaki ndani ya lengo la BoT la asilimia tatu hadi tano. Kwa wastani, ulikuwa asilimia 3.3 Tanzania Bara na asilimia 4.5 Zanzibar, hali iliyochangiwa na utulivu wa bei za chakula pamoja na kiwango cha ubadilishaji fedha.

Hata hivyo, Benki Kuu imeonya kuwa ongezeko la gharama za nishati na usafirishaji linaweza kuongeza shinikizo la mfumuko wa bei katika miezi ijayo.

Katika sekta ya benki, hali imeendelea kuwa imara ambapo kiwango cha mikopo chechefu kimeshuka hadi asilimia 2.9, chini ya kiwango kinachokubalika kisheria, huku benki zikiendelea kuwa na mtaji wa kutosha na ukwasi wa kuridhisha.

Kwa upande wa sekta ya nje, nakisi ya akaunti ya sasa imepungua hadi asilimia 2.2 ya Pato la Taifa (GDP), ikichangiwa na kuongezeka kwa mauzo ya nje ya dhahabu, mazao ya kilimo na huduma za utalii.

Zanzibar nayo imeendelea kufanya vizuri, ikirekodi ziada ya akaunti ya sasa kutokana na mapato ya utalii.

Aidha, akiba ya fedha za kigeni imefikia zaidi ya dola za Marekani bilioni 6.2, kiwango kinachoweza kugharamia uagizaji wa bidhaa kwa karibu miezi mitano, juu ya viwango vya kikanda.

Kwa upande wa mapato ya serikali, makusanyo ya kodi yamevuka malengo kutokana na kuimarika kwa usimamizi na utii wa walipakodi, huku matumizi ya serikali yakiendelea kubaki ndani ya mipaka ya rasilimali zilizopo.

Hata hivyo, MPC imeonya kuwa bado kuna hatari zinazoikabili uchumi.

“Tishio kubwa kwa matarajio ya uchumi ni mzozo unaoendelea Mashariki ya Kati. Endapo utaongezeka, unaweza kuongeza mfumuko wa bei na kupunguza kasi ya ukuaji wa uchumi duniani na nchini,” alisisitiza Dkt. Kayandabila. 









Top News