Na Pamela Mollel, Arusha
Habari njema kwa wakazi wa Arusha! Halmashauri ya Wilaya ya Arusha imependekeza bajeti ya shilingi bilioni 75.4 kwa mwaka wa fedha ujao, hatua inayotajwa kuwa chachu ya maendeleo katika sekta mbalimbali ikiwemo elimu, miundombinu na huduma za kijamii.
Bajeti hiyo inatajwa kuwa na neema kubwa kwa wanafunzi wapya zaidi ya 20,000 wanaotarajiwa kujiunga na kidato cha kwanza mwakani.
Akizungumza katika kikao cha Baraza la Madiwani kilichofanyika juzi, Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo, Baraka Simon, alisema bajeti hiyo imegawanyika katika sehemu kuu mbili.
Alifafanua kuwa kati ya bilioni 75.4 zilizopendekezwa, fedha hizo zimeelekezwa katika miradi ya maendeleo, huku mapato ya ndani yakitarajiwa kuwa shilingi bilioni 9.2.
“Bilioni 75.4 ni kwa ajili ya miradi ya maendeleo, lakini kwa upande wa mapato ya ndani ni bilioni 9.2. Tuna imani kubwa sana na bajeti hii na tunajua italeta mafanikio makubwa sana na itakuwa rafiki kwa wananchi,” alisema.
Katika hatua nyingine, alisema bajeti hiyo imelenga pia kuandaa vyumba zaidi ya 200 vya madarasa kwa ajili ya wanafunzi wapya wa kidato cha kwanza watakaoanza masomo mwakani.
Alieleza kuwa mabadiliko yanayotarajiwa katika mfumo wa elimu yataongeza idadi ya wanafunzi wa kidato cha kwanza, baada ya wanafunzi wa darasa la sita kuhitimu na kujiunga na ngazi hiyo sambamba na wenzao wengine.
“Mwakani kutakuwa na mabadiliko ya mfumo wa elimu. Wanafunzi wa darasa la sita wakimaliza watajiunga na kidato cha kwanza, lakini hata hao wengine nao wanatakiwa kuingia kidato cha kwanza. Tumejipanga vyema,” aliongeza.
Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Mlangarini, Emanuel Mrema, alisema wanashukuru kwa bajeti hiyo kwani imegusa nyanja zote muhimu zinazohitajika katika jamii.
Alisema pamoja na kuwepo kwa changamoto katika baadhi ya kata, kupitia bajeti hiyo vijiji vyote vitanufaika na miradi ya maendeleo itakayotekelezwa katika mwaka wa fedha ujao.
Kwa ujumla, bajeti hiyo imeibua matumaini mapya kwa wananchi wa Wilaya ya Arusha, huku matarajio makubwa yakiwekwa katika utekelezaji wake ili kuleta matokeo chanya yanayokusudiwa.



























.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)



















