DAR ES SALAAM
WADAU wa sekta ya ukarimu na utalii wameeleza umuhimu unaoongezeka wa vyakula, mvinyo na uzoefu wa kiutamaduni katika kuimarisha nafasi ya Tanzania kama kivutio cha utalii.

Kauli hiyo ilitolewa wakati wa hafla ya maonesho ya mvinyo wa Afrika Kusini iliyofanyika jijini Dar es Salaam, ambapo wawakilishi wa sekta hiyo walisema uzoefu wa ukarimu na burudani unazidi kuwa sababu muhimu inayowaongoza watalii kuchagua maeneo ya kutembelea na namna wanavyotumia fedha zao wanapokuwa safarini.

Meneja wa Masoko wa Afrika wa Wines of South Africa, Matome Mbatha, alisema maboresho ya miundombinu ya utalii nchini Tanzania, ukuaji wa sekta ya ukarimu na kuongezeka kwa mtindo wa maisha ya kisasa mijini vinafungua fursa zaidi za kuvutia watalii wa kimataifa.

Alisema uzoefu unaojumuisha vyakula, mvinyo, utamaduni, muziki na burudani za usiku sasa unachangia kwa kiasi kikubwa ukuaji wa utalii duniani na unaweza kuisaidia Tanzania kuongeza ushindani wake katika sekta hiyo.

Mbatha alisema taasisi hiyo imekuwa ikifanya kazi nchini Tanzania kwa kipindi cha miaka mitano iliyopita kwa kushirikiana na hoteli, migahawa, waagizaji na wasambazaji wa bidhaa ili kukuza utamaduni wa matumizi ya mvinyo pamoja na kuboresha viwango vya huduma katika sekta ya ukarimu.

Alisema sehemu ya mpango huo ni kutoa mafunzo kwa wafanyakazi wa hoteli na migahawa kuhusu uelewa wa mvinyo na huduma kwa wateja ili kuboresha uzoefu wa wageni wanapotembelea maeneo mbalimbali ya huduma.

Kwa mujibu wake, Wines of South Africa pia imeanzisha programu za mafunzo maalum na kozi za bure za mtandaoni zinazolenga kuongeza ujuzi kwa wafanyakazi wa sekta ya ukarimu pamoja na kuwajengea vijana fursa za ajira katika sekta hiyo.

Alisema Afrika Mashariki inaendelea kuwa soko muhimu la matumizi ya mvinyo, huku Tanzania ikiwa miongoni mwa masoko yanayokua kwa kasi kutokana na kuongezeka kwa shughuli za utalii na upanuzi wa huduma za kisasa za ukarimu.

Kwa upande wake, Kaimu Balozi wa Afrika Kusini nchini Tanzania, Frans van Aardt, alisema matukio ya utalii na ukarimu yanasaidia kuimarisha mahusiano ya kiutamaduni na kiuchumi kati ya nchi kupitia fursa za biashara, uwekezaji na mwingiliano wa kijamii.

Alisema ushirikiano kati ya Tanzania na Afrika Kusini unaendelea kukua katika sekta mbalimbali zikiwemo utalii, madini, benki na mawasiliano ya simu, ukiungwa mkono na maono ya pamoja ya ukuaji wa uchumi na maendeleo ya kikanda.

Tukio hilo lililofanyika katika Delta Hotels Dar es Salaam lilikuwa sehemu ya ziara ya Wines of South Africa katika Afrika Mashariki inayolenga kuwaunganisha wazalishaji wa mvinyo, wadau wa sekta ya ukarimu na watumiaji katika ukanda huo.







Na Karama Kenyunko Michuzi Tv
WATAALAMU wamewahimiza wanafunzi wa tiba na madaktari bingwa wa watoto kujikita katika fani ya Pediatric Rheumatology (Magonjwa ya Mfumo wa Kinga na maungio yanayoathiri watoto) ili kupunguza uhaba mkubwa wa wataalamu katika nchi na barani Afrika kwa ujumla.

Licha ya kuongezeka kwa magonjwa hayo, takwimu zinaonyesha kuwa Afrika yenye zaidi ya watu bilioni 1.4 ina wataalamu wasiozidi 20 wa magonjwa hayo ya watoto (pediatric rheumatologists) katika bara zima, huku Tanzania ikiwa na mtaalamu mmoja tu, hali ambayo wataalam wanaieleza kuwa ya kutia wasiwasi kwa watoto wanaougua magonjwa ya kinga mwilini na ya viungo.

Kimataifa, tafiti zinaonyesha kuwa magonjwa ya rheumatic, ambayo huainishwa kama magonjwa adimu, huathiri watoto kati ya mmoja hadi wanne kwa kila watoto 1,000 duniani.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa sita wa magonjwa ya viungo na misuli kwa watoto wa Afrika lililofanyika leo Mei 14, 2026 kwa mfumo wa mseto jijini Dar es Salaam , Profesa Francis Furia kutoka Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS) alisema uhaba wa wataalamu umesababisha watoto wengi kuchelewa kugundulika na kukosa matibabu kwa wakati, jambo linalozidi kuzorotesha hali zao za kiafya.

Profesa Furia, ambaye ni daktari wa watoto, alisema kuongeza idadi ya wataalamu wa pediatric rheumatology kutaimarisha kwa kiasi kikubwa huduma za afya kwa watoto na kusaidia kuokoa maisha ya wagonjwa wengi wanaoathiriwa na magonjwa hayo.

“Kwa sababu ya changamoto hizi, tunaendelea kusisitiza umuhimu wa kuongeza idadi ya wataalamu katika fani hii. Kupitia kongamano hili la sita, tumewapatia mafunzo madaktari wanaoendelea na mafunzo na madaktari wa watoto ili waweze kutambua dalili mapema na kutoa matibabu kwa wakati,” alisema Profesa Furia.

Pia aliipongeza serikali kwa hatua inazochukua katika kuimarisha huduma hizo katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH).

“Tanzania imeanza kupiga hatua. Uwekezaji mkubwa umefanyika Muhimbili ambapo huduma hizi zinatolewa. Maabara zimeboreshwa na vipimo vingi ambavyo awali vilikuwa vikifanyika nje ya nchi sasa vinafanyika hapa nchini,” alieleza.

Aliongeza kuwa hospitali hiyo imeanzisha kliniki maalum kwa watoto wanaougua magonjwa hayo, ambapo zaidi ya watoto 50 kutoka mikoa mbalimbali wanapata matibabu.

“Hii ni hatua muhimu kuhakikisha watoto hawa wanapata huduma wanazostahili,” alisema.

Akizungumza kwa niaba ya Mganga Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam wakati wa ufunguzi wa kongamano hilo, Dkt. Gunini Kamba alisema serikali iko tayari kuendelea kushirikiana na wadau mbalimbali katika kutoa fursa za elimu, ikiwemo udhamini wa masomo hasa katika fani adimu za tiba.

“Tunahamasisha wote wenye nia na uwezo kujitokeza na kusomea fani hizi maalum ili kusaidia kuboresha huduma za afya nchini,” alisema.

Rais wa Jumuiya ya Madaktari wa Watoto wa Umoja wa Afrika dhidi ya Magonjwa ya Rheumatism (PAFLAR), Dkt. Ayodele Faleye alizitaka serikali za Afrika kusaidia udhamini wa madaktari wa watoto wenye nia ya kujikita katika pediatric rheumatology.

“Kuna uhitaji mkubwa wa kuwazalisha wataalamu zaidi katika fani hii,” alisisitiza.

“Tunahitaji kwa dharura kuimarisha uwezo wa maabara. Katika nchi nyingi za Afrika, sampuli za damu bado hutumwa nje ya bara kwa ajili ya uchunguzi. Hii husababisha kuchelewa kwa matokeo ya uchunguzi na matibabu, ambapo wakati mwingine huchukua siku 7 hadi 10.”

Aliongeza kuwa kuimarishwa kwa maabara za ndani kutasaidia utambuzi wa haraka na kuanza matibabu kwa wakati.

Pia alisema upatikanaji wa dawa muhimu bado ni changamoto kubwa, akieleza kuwa dawa nyingi huagizwa kutoka nje ya Afrika, jambo linalofanya ziwe ghali na wakati mwingine kukosekana.

“Uingiliaji wa serikali ni muhimu kuhakikisha dawa zinapatikana kwa uhakika na kwa bei nafuu,” alisisitiza.





Waziri wa Afya, Mhe. Mohamed Mchengerwa leo Mei 14, 2026 amekutana na Kaimu Balozi wa Marekani Nchini Andrew Lentz na kufanya majadiliano kuhusu Mkataba Mpya wa Ushirikiano (MoU) wa Afya kati ya Marekani na Tanzania

Mkutano huo uliofanyika jijini Dar es Salaam katika Ofisi ya Waziri wa Afya, ulisisitiza dhamira ya pamoja ya nchi zote mbili katika kuimarisha usalama wa afya, huku ukilenga kuboresha mashirikiano katika maeneo mbalimbali ya Sekta ya Afya ikiwemo huduma za tiba, mafunzo kwa wataalamu pamoja na uimarishaji wa mifumo ya afya nchini

Akizungumza katika kikao hicho, Mheshimiwa Mchengerwa amefafanua kuwa Serikali itaendelea kuthamini ushirikiano mzuri ulioimarika kwa muda mrefu baina ya Tanzania na Marekani kwenye huduma za afya.

Amesema kupitia mashirikiano hayo, Tanzania imeendelea kunufaika katika maeneo mbalimbali ikiwemo mapambano dhidi ya magonjwa ya mlipuko, huduma za mama na mtoto pamoja na ujenzi wa uwezo kwa wataalam wa afya.

Aidha, ujumbe wa Ubalozi wa Marekani umeeleza utayari wao wa kuendelea kushirikiana na Serikal a Tanzania katika kutekeleza miradi mbalimbali ya afya yenye lengo la kuboresha huduma kw: wananchi.

Kikao hicho pia kilijadili namna ya kuongeza ushirikiano katika matumizi ya teknolojia za kisasa kwenye sekta ya afya, ukuaji wa ujenzi wa viwanda na vifaa tiba, tafiti za kitabibu pamoja na kubadilishana uzoefu kati ya wataalamu wa afya wa Tanzania na Marekani.

Katika majadiliano hayo upande wa Serikali ya Tanzania uliongozwa na Mheshimiwa Mchengerwa, Katibu Mkuu, Daktari Seif Shekalaghe, Naibu Katibu Mkuu anayeshughulikia Dawa na Vifaa Tiba Emmanuel Tayari, Mganga Mkuu wa Scrikali, Daktari Grace Magembe na Mkurugenzi wa Sheria wa Wizara, Rahibu Mashombo, huku Ujumbe Wa Ubalozi ukiongozwa na Kaimu Balozi wa Marekani Nchini Andrew Lentz na Maafisa waandamizi wa Ubalozi huo










NA MWANDISHI WETU

 BARAZA la Wadhamini la Chama Cha Mapinduzi (CCM) limeeleza kuridhishwa na utekelezaji wa   miradi inayotekelelezwa  kwa   ubia baina ya Chama, jumuiya zake na wadau .

Hayo yameelezwa na wajumbe wa baraza hilo katika ziara ya kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo  mkoani Dar es salaam leo,  inayotekelezwa na CCM,  Jumuiya ya Wazazi na Umoja wa wanawake Tanzania (UWT) .

Akizungumza baada ya ziara  hiyo ,Makamu Mwenyekiti wa Baraza la Wadhamini  la CCM, Vuai Ali Vua,  amesema   CCM ni  Chama cha siasa   kinacho taka kujitegemea  hivyo   ili kufikia azama hiyo  kinafanya shughuli za kisiasa na kiuchumi.

"Hivyo  wito kwa watendaji wetu wa Chama  kuanzia  ngazi za shina, tawi kata, wilaya mkoa na taifa  ni kutumia fursa zilizopo katika taifa letu kupromoti  miradi ya CCM kuongeza pato la Chama,"alisema Vuai.

 Ameeleza  ni wajibu wa watendaji wa CCM  na jumuiya zake kuwa wabunifu  wa kiuchumi na kisiasa  kwani ndiyo aina ya watendaji ambao chama kintegemea kuwa nao  katika kipindi hiki.

Akizungumzia a mradi wa jengo la kitega uchumi la  Jumiuya ya Wazazi Tanzania katika eneo la Ilala Mchikichini  Kiwanja 2C na 2B wenye thamani  ya sh. bilioni 2.3, Vuai  amesema baraza limeridhishwa na utekelezaji wa mradi huo  ambao umesuasua kwa miaka mingi sasa.

Ameshauri Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Wazazi  Tanzania, Ally  Hapi,  kukaa na Kampuni ya MCL ambaye ni mwekezaji wa mradi huo  wa ghorofa  moja unaohusisha , nyumba za makazi na ofisi  kuongeza  ghorofa zaidi kutoka ghorofa moja iliyopo.

Awali Mjumbe wa Bodi hiyo, Kapten mstaafu John Chiligati, alishauri  kwa kuwa mradi huo ulikusudiwa kujenga ghorofa 20 ambapo msingi wake  unaweza kubeba ghorofa hizo  ni vyema utekelezaji ukaendelea.

Pia, Mjumbe wa Bodi hiyo, Andrew Chenge, ameshauri  Jumuiya ya Wazazi kukaa vyema na wawekezaji   Kampuni ya MCL  kuhakikisha uwekezaji huo unakuwa endelevu na haushii hapo ili ulete tija zaidi.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi Tanzania,  Fadhili Maganya, amesema  kukamilika kwa jengo hilo kumechukua muda mrefu kutokana na migogoro 'mazonge'  mbalimbali  ambayo hata hivyo ilitatuliwa na utekelezaji kufanyika hatimaye jengo kukamilika.

Katibu wa Jumuiya hiyo,  Ally Hapi, amesema amepokea ushauri na maelekezo ya baraza hilo hususan kukaa na Kampuni ya Uwekezaji ya MCL kwaajili ya kuendeleza ujenzi  wa jengo hilo   kujengwa kwa zaidi ya  ghorofa moja .

Bodi hiyo pia ilikagua maendeleo ya ujenzi wa jengo la kitega uchumi la UWT  linalojengwa  katika eneo  la SUWATA, jijini Dar es Salaam kwa gharama ya sh. bilioni 6  na kupongeza umoja huo  kwa hatua hiyo kubwa.


 Dereva wa Bodaboda Auawa Morogoro

Dereva bodaboda aliyefahamika kwa jina la Ally Kambi (24), mkazi wa Kingolwira Manispaa ya Morogoro, anadaiwa kuuawa na watu wasiojulikana baada ya kukodi huduma yake ya usafiri, kisha kuporwa pikipiki yake.

Tukio hilo linasadikika lilitokea katika eneo la Mkambarani Wilaya ya Morogoro, ambapo mwili wa marehemu ulipatikana porini ukiwa na majeraha.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Andrew Kantimbo, amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kusema jeshi la polisi linaendelea na uchunguzi ili kuwabaini waliohusika na mauaji hayo.

Akizungumzia tukio hilo na Moja ya chomba Cha Habari baba mkubwa wa marehemu aliyejitambulisha kwa jina la Shukuru Msonga amesema Ally aliondoka Mei 11, 2026 majira ya usiku baada ya kukodiwa na mtu asiyejulikana, lakini hakurejea nyumbani.

Msonga amesema baada ya kijana huyo kutorejea kwa siku nzima, familia ilitoa taarifa kwa Serikali ya mtaa na kituo cha polisi, ambapo juhudi za kumtafuta zilianza mara moja.

“Tulihangaika kumtafuta maeneo mbalimbali, tulifika hata hospitali na kutoa taarifa kwenye vijiwe vya bodaboda. Hatimaye jana asubuhi tukapata taarifa kuwa kuna mwili umeonekana porini,” amesema Msonga.

Amesema yeye pamoja na ndugu wengine walipofika eneo la tukio waliutambua mwili huo kuwa ni wa Ally Kambi. Mwili huo ulikuwa na majeraha, huku pembeni kukiwa na fimbo kubwa (gongo) pamoja na fulana iliyokuwa imelowa damu.

Jeshi la polisi linaendelea na uchunguzi wa tukio hilo huku juhudi za kuwatafuta watuhumiwa zikiendelea.



📍TRA yawawekea mkakati rafiki wa Kodi

Na MASHAKA MHANDO, Tanga


MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Tanga, imebainisha kuwa wanawake nchini wanamiliki asilimia 54 ya biashara ndogo, za kati na ndogo (MSMEs), hali inayolazimu kuwepo kwa mifumo rafiki ya kodi itakayochochea ukuaji wa sekta hiyo bila hofu ya vikwazo.

Kauli hiyo imetolewa leo Mei 14, 2026, na Meneja wa TRA Mkoa wa Tanga, John Castro wakati akifungua Kongamano la Jukwaa la Wanawake na Kodi lililofanyika katika ukumbi wa Regal Naivera Hotel jijini hapa.

John alisema takwimu za hivi karibuni zinaonyesha mchango mkubwa wa wanawake katika uchumi, ambapo ushiriki wao katika nguvu kazi unakadiriwa kufikia takribani asilimia 80 kwa mwaka wa fedha 2024/2025, jambo linalowafanya kuwa mhimili mkuu wa mapato ya ndani.

Jukwaa la Wanawake na Kodi

Meneja huyo alifafanua kuwa kuanzishwa kwa jukwaa hilo ni hatua ya kihistoria yenye lengo la kuwapa wanawake elimu sahihi, kusikiliza changamoto zao, na kujenga uaminifu utakaohamasisha ulipaji kodi kwa hiari badala ya kutumia nguvu.

"Tunatambua kuwa mwanamke akisimama kiuchumi, familia inaimarika na Taifa linapiga hatua. TRA imejikita kuboresha huduma kwa weledi na uwazi ili mwanamke ajisikie salama na anaheshimiwa anaposhiriki katika mfumo wa kodi," alisema John.




Kodi na Miradi ya Kimkakati

John alisisitiza kuwa kodi ndiyo injini inayogharamia miradi ya kimkakati nchini ikiwemo afya, elimu, barabara na maji, hivyo mwanamke anayelipa kodi anakuwa mshirika wa moja kwa moja wa Serikali katika ujenzi wa Taifa.

Aidha, aliishukuru Serikali ya Mkoa wa Tanga chini ya Mhe. Balozi Dkt. Batilda Burian na wadau wa maendeleo kama GIZ, kwa kuweka mazingira yanayowawezesha kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi na kupata elimu ya kodi.

Wito kwa Wadau na Taasisi za Fedha

Katika kongamano hilo, TRA imetoa wito kwa taasisi za kifedha kushirikiana na Mamlaka hiyo wakati wa kutoa mikopo kwa wajasiriamali wanawake, ili waweze kupewa elimu ya kodi sambamba na mitaji, jambo litakalosaidia biashara zao kuimarika na kuwa endelevu.

Pia, aliwataka wanawake wote mkoani Tanga kujisajili katika mfumo wa kodi na kutumia madawati ya uwezeshaji biashara yaliyopo katika kila ofisi ya TRA ili kupata ushauri wa kitalamu wa kibiashara.

Mmoja ya washiriki wa kongamano Hilo, kutoka kampuni ya Maluu Smart Production, Hadija Mohamed, ameipongeza Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) mkoani Tanga kwa kuanzisha jukwaa hilo, akisema limekuwa mkombozi katika kufungua macho ya wanawake wajasiriamali kuhusu mnyororo wa kodi na fursa za kibiashara. Hadija amebainisha kuwa elimu waliyoipata itawasaidia kuendesha biashara zao kwa weledi na kuondoa hofu ya awali waliyokuwa nayo dhidi ya kodi, jambo litakalopelekea uzalishaji wenye tija na kufuata sheria za nchi kitalamu.

Aidha, Hadija amesisitiza kuwa kupitia mafunzo hayo, Maluu Smart Production imejipanga kuwa balozi wa utii wa kodi kwa hiari, huku akiiomba TRA kuendelea kutoa huduma za ushauri wa karibu kwa viwanda vidogo ili viweze kukua na kufikia soko la kimataifa. Amesema kuwa kutambuliwa kwa mchango wa mwanamke katika uchumi kupitia kongamano hilo ni ishara tosha ya ushirikiano wa dhati kati ya Serikali na sekta binafsi katika kukuza mapato ya ndani na maendeleo ya kijamii.







Na Aron Msigwa – Nairobi, Kenya

Mkuu wa Kamandi ya Jeshi la Nchi Kavu, Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), Meja Jenerali Fadhili Omary Nondo, ameungana na Maafisa Wakuu wa Majeshi na viongozi mbalimbali kutoka nchi Wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) akimwakilisha Mkuu wa Majeshi ya Tanzania, Jenerali Jacob John Mkunda katika ufunguzi rasmi wa zoezi la 14 la pamoja la Vituo vya Uamrishaji vya Kijeshi vya Nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki lijulikanalo kama Ushirikiano Imara 2026, uliofanyika leo Mei 14, 2026 jijini Nairobi, Kenya.

Zoezi hilo kubwa la kijeshi limekusanya washiriki kutoka nchi za Kenya, Tanzania, Uganda, Burundi, Rwanda, Sudani Kusini na Somalia kwa lengo la kuimarisha utayari, ushirikiano na uwezo wa vikosi vya ulinzi vya Jeshi, Polisi, Magereza, Uhamiaji, Zimamoto, Wizara na taasisi za kiraia katika kukabiliana na changamoto za kiusalama zinazolikabili eneo la Afrika Mashariki.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa zoezi hilo, Makamu Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi ya Kenya (VCDF), Luteni Jenerali John Mugaravai Omenda, amesisitiza umuhimu wa nchi wanachama wa EAC kuendelea kuimarisha mshikamano, ushirikiano na maandalizi ya pamoja katika kukabiliana na vitisho vinavyojitokeza, majanga mbalimbali pamoja na changamoto za kiusalama zinazoweza kuhatarisha amani na utulivu wa kikanda.

Zoezi la Ushirikiano Imara 2026 limejengwa katika mazingira ya kinadharia ya nchi ya kufikirika ya “Jamhuri ya Pwani,” inayokabiliwa na mgogoro wa kisiasa huku likiangazia Operesheni za kusaidia Amani (PSO), Kupambana na Ugaidi (CT), Kupambana na Uharamia Baharini (CP) pamoja na Usimamizi wa Maafa (DM).

Katika mazoezi hayo, vikosi kutoka Tanzania, Kenya, Burundi, Rwanda, Uganda, Somalia na Sudani Kusini vitaonesha umahiri kupitia mafunzo mbalimbali katika eneo la Mawasiliano ya kimkakati, kubadilishana taarifa za usalama, uratibu wa operesheni, doria katika maeneo ya mijini pamoja na mbinu za utendaji katika mazingira hatarishi.

Mazoezi hayo yanalenga kuonesha kiwango cha juu cha taaluma, nidhamu na uwezo wa kiutendaji wa vikosi shiriki, sambamba na kuimarisha uwezo wa pamoja katika kulinda amani na usalama wa kikanda mipango ya pamoja ya kuzuia migogoro, kuimarisha utayari wa kukabiliana na majanga na kuboresha mifumo ya utoaji wa misaada ya kibinadamu katika ukanda huo.

Zoezi la Ushirikiano Imara 2026 linafanyika kwa kuzingatia Itifaki ya Ushirikiano wa masuala ya Ulinzi ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, inayolenga kuimarisha ushirikiano kati ya nchi wanachama kupitia upangaji na utekelezaji wa operesheni za pamoja zinazohusisha vyombo vya ulinzi na wadau wa kiraia.

Hafla hiyo ya ufunguzi imehudhuriwa pia na Msimamizi Mkuu wa zoezi hilo (Chief Umpire) ambaye pia ni Kiongozi wa kikosi cha Tanzania, Brigedia Jenerali Maneno Almasi Mabakila, Maofisa Waandamizi kutoka Jeshi la Polisi, Uhamiaji, Magereza, Wizara na Taasisi za Kiraia wanaoshiriki zoezi hilo.










Na Belinda Joseph-Dodoma.

Masuala ya usawa wa kijinsia, uwezeshaji wa wanawake na makundi maalum pamoja na mapambano dhidi ya mfumo dume yameendelea kupewa uzito nchini, huku wadau mbalimbali wakisisitiza umuhimu wa jamii kushiriki kwa pamoja kujenga mazingira yenye haki na usawa kwa wote.

Hayo yamejadiliwa Mei 14, 2026 Jijini Dodoma katika mjadala ulioandaliwa na Aga Khan Foundation kupitia mradi wa Tuinuke Pamoja, uliowakutanisha viongozi wa dini, maafisa maendeleo ya jamii, wazee wa mila pamoja na vikundi vya wanawake vinavyowezeshwa na mradi huo kwa Wilaya za Bahi, Dodoma Jiji na Chamwino.

Akizungumza katika mjadala huo, Zaibu Mmari ambaye ni mratibu wa masuala ya kijinsia wa Aga Khan Foundation Makao Makuu Dar es Salaam, amesema lengo la mradi huo ni kuchochea usawa wa kijinsia katika jamii, kujenga uelewa wa pamoja, kuimarisha mshikamano na kuleta mahusiano bora kupitia elimu na ushirikiano wa kijamii.

Amesema tafiti mbalimbali zinaonyesha kuwa wanawake na wasichana barani Afrika wameachwa nyuma kwa muda mrefu katika nyanja mbalimbali za maendeleo, jambo lililosababisha mradi huo kuelekeza nguvu kubwa kwa wanawake na wasichana kwa zaidi ya asilimia 70.

“Tunataka kuhakikisha kwamba usawa unaendana na haki, Fursa lazima zigawanywe kwa kuzingatia mahitaji ya kila kundi katika jamii, Pia tunawahimiza viongozi wa dini kutumia madhabahu na mimbari kufundisha kuhusu usawa wa kijinsia, kupinga mfumo dume na kukemea fikra mgando.”

Ameeleza kuwa mradi wa tuninuke pamoja unaratibiwa na Aga Khan Foundation ambayo ipo chini ya Aga Khan Development Network ambao ni mtandao wa maendeleo unaojihusisha na shughuli za kiuchumi, kijamii na kitamaduni chini ya jumuiya ya Waislamu wa Ismailia. Kupitia Aga Khan Foundation, taasisi hiyo imekuwa ikifanya kazi moja kwa moja na jamii katika kutambua changamoto na kushirikiana kutafuta suluhisho la pamoja.

Mradi wa Tuinuke Pamoja unafadhiliwa na Ubalozi wa Ireland nchini Tanzania na unatekelezwa kwa kipindi cha miaka mitatu kuanzia Julai 2024 hadi Juni 2027 katika Halmashauri zote za Mkoa wa Dodoma.

Afisa Mradi wa Tuinuke Pamoja katika Halmashauri ya Wilaya ya Bahi, Erick Maurid, alisema mradi huo unafanya kazi kwa karibu na vikundi vya wanawake, vijana pamoja na makundi maalum katika jamii ili kuvijengea uwezo wa kiuchumi na kijamii.

Amesema katika mwaka wa kwanza wa utekelezaji, mradi ulifika Wilaya za Kondoa DC, Kondoa TC na Chemba, huku mwaka wa pili ukihusisha Wilaya za Bahi, Dodoma Jiji na Chamwino na mwaka wa tatu unatarajiwa kufikia Wilaya za Kongwa na Mpwapwa.

Ameeleza kuwa vikundi hivyo hutakiwa kusajiliwa kupitia maafisa maendeleo ya jamii katika halmashauri husika, huku mradi ukiwasaidia katika maeneo ya elimu ya biashara, ujasiriamali na usawa wa kijinsia.

“Mjadala huu unalenga kujenga mazingira bora katika jamii kwa kujadili masuala ya uwezeshaji wa wanawake kiuchumi, elimu, utawala bora, HIV pamoja na haki za watu wenye ulemavu”.

Aidha amesema wanawake, vijana, wazee na watu wenye ulemavu bado wanakabiliwa na changamoto mbalimbali zinazowakwamisha kufikia maendeleo, hivyo kuna haja ya kuweka mikakati madhubuti ya kuwawezesha ili waweze kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya jamii.

Katika mjadala huo, wazee wa mila kutoka Halmashauri za Bahi, Chamwino na Dodoma Jiji wamesisitiza umuhimu wa kulea watoto katika misingi ya usawa bila upendeleo wa kijinsia.

Wamesema viongozi wa serikali za mitaa wanapaswa kuwapa nafasi ya kutoa mawaidha katika mikutano ya vijiji ili kusaidia kurejesha maadili katika jamii, huku wakitoa rai kwa wazazi kuhakikisha watoto wa kike hawarubuniwi na kuingia katika mimba za utotoni.

Kwa upande wake, Ester Athanas kutoka Wilaya ya Bahi, amesema changamoto kubwa inayojitokeza vijijini ni mgawanyo usio sawa wa mali na urithi kati ya watoto wa kike na wa kiume.

Aidha ameeleza jinsi wanawake wengi ambavyo bado wananyimwa nafasi za maamuzi na kudharauliwa katika jamii kutokana na imani potofu na mifumo kandamizi.

“Ni muhimu kuondoa ukuta wa usiri kati ya mzazi na mtoto ili watoto waweze kueleza changamoto wanazokutana nazo kwa uhuru. Pia sheria ziangaliwe upya ili watoto wa ndani na nje ya ndoa waweze kupata haki sawa ya urithi.”

Naye Valentino Kibaja Mchungaji kutoka Wilaya ya Chamwino amewataka viongozi wa dini kuendelea kuhimiza ibada, maadili na elimu kwa usawa kwa watoto wa kike na wa kiume.

Amesema pia kuna umuhimu wa kuongeza ushirikishwaji wa viongozi wa dini katika mijadala ya kijamii ili kusaidia kujenga jamii yenye usawa, amani na mshikamano.

Mjadala huo umeonekana kuwa jukwaa muhimu la kuwakutanisha wadau mbalimbali kujadili namna bora ya kuondoa changamoto za kijinsia na kuhakikisha makundi yote katika jamii yanapata haki, fursa na ushiriki sawa katika maendeleo.










Top News