MRADI wa ECOFISH unaotekelezwa kwa ushirikiano kati ya Serikali ya Tanzania na Denmark kupitia Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na Shirika la Denmark la Maendeleo ya Kimataifa (DANIDA), unaendelea kuboresha shughuli za uvuvi kwa jamii ya Pwani na kuimarisha huduma za tahadhari za mapema za hali ya hewa nchini.

Katika utekelezaji wa mradi huo, wataalamu kutoka TMA walikutana na wavuvi pamoja na wakulima wa Mwani kwa lengo la kujionea hali halisi ya shughuli zao za kiuchumi na changamoto zitokanazo na mabadiliko ya hali ya hewa wanazokabiliana nazo, sambamba na kutoa elimu kuhusu matumizi sahihi ya taarifa za hali ya hewa katika shughuli za uvuvi na kilimo cha Mwani. Ziara hiyo iliambatana na semina maalum iliyowakutanisha wavuvi na wakulima wa Mwani ikiwa ni sehemu ya juhudi za mradi huo katika kuongeza uelewa wa jamii kuhusu umuhimu wa matumizi ya taarifa za hali ya hewa katika kufanya maamuzi sahihi na salama.

Akizungumza katika semina hiyo, Mtaalamu wa Hali ya Hewa kutoka TMA na msimamizi wa mradi, Dkt. Sarah Emerald Osima, alisema mradi wa ECOFISH una mchango mkubwa katika kuimarisha huduma za hali ya hewa na ustahimilivu wa jamii za Pwani kupitia tafiti, elimu na teknolojia za tahadhari za mapema.

Dkt. Sarah aliendelea kusema mradi huo pia umewezesha udhamini wa masomo kwa wanafunzi saba wa shahada za uzamili na uzamivu kutoka Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi Tanzania (TAFIRI), Taasisi ya Sayansi za Bahari ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (IMS) pamoja na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), ambapo mmoja wao ni mfanyakazi wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA). Alisema hatua hiyo inalenga kujenga wataalamu watakaosaidia sekta ya uvuvi na hali ya hewa kwa siku zijazo.

Aidha, wananchi wa kisiwani hapoo wamepongeza mradi huu wa ECOFISH na TMA kwa kuwapatia elimu hiyo, wakisema imewasaidia kuelewa na kutumia taarifa za hali ya hewa katika kupanga shughuli zao za uvuvi.

“Sasa tunajua umuhimu wa kutafuta na kutumia taarifa za hali ya hewa, jambo ambalo hapo awali tulikuwa tunalifanya kwa uelewa mdogo. Kwa sasa tumejifunza mambo mengi ikiwemo namna ya kutafsiri taarifa hizo kama zinavyotolewa na wataalamu,” alisema Afisa Uvuvi kutoka Wilaya ya Wete, Ndugu,Suleiman Ali Amadi.

Na; Mwandishi Wetu Arusha
OFISI ya Makamu wa Rais inatarajiwa kuzindua Programu ya Kitaifa ya Mageuzi ya Kimkakati ya Mazingira Endelevu Tanzania katika kilele cha Siku ya Mazingira Duniani (WED) ambapo kitaifa itafanyika jijini Dodoma, Juni 5, 2026.

Akizungumza katika uzinduzi wa usafi wa Mazingira kuelekea siku hiyo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni alisema lengo ni kuhakikisha Tanzania inakuwa nchi ya mfano duniani katika suala la Uhifadhi na Utunzaji wa Mazingira.

Alisema Programu hiyo inalenga kutekeleza Dira, 2050 hususan nguzo ya tatu kuhusu Uhifadhi wa Mazingira na Ustahimilivu wa Mabadiliko ya Tabianchi ikiwa na lengo la kupanda miti bilioni 2 kwa mwaka, kuimarisha Biashara ya Kaboni, Uanzishaji wa Bustani za Kijani katika Miji na shughuli zingine za Kijani.

“Pia program hii inatarajia kuongeza ajira zinazoweza kufikia zaidi ya elfu ishirini na tano (25,000) ifikapo 2030 kupitia sekta za taka, misitu, kaboni na nishati safi,”alisema Mhe. Masauni.

Alifafanua kuwa tukio hilo ni sehemu ya juhudi za Kitaifa na Kimataifa za kulinda mazingira, kupambana na athari za mabadiliko ya tabianchi na kujenga jamii yenye afya na ustahimilivu.

Aidha, alileza Dira, 2050 imeweka maono ya Taifa kuwa hadi kufikia mwaka 2050 Tanzania iwe kinara katika matumizi endelevu ya rasilimali, Taifa linalotumia taka kama malighafi kwa manufaa ya kiuchumi na Taifa kinara katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi kwa kuimarisha ustahimilivu na uendelevu wa mazingira.

“Juhudi zinahitajika ili kutekeleza shughuli za mazingira kwa njia jumuishi inayohusisha makundi yote ya kijamii bila kujali jinsia au umri. Kwa jiji la Arusha, tafiti za mwaka 2020 zinaonesha kuwa jiji linazalisha takribani tani 550 za taka ngumu kwa siku, ambapo zaidi ya asilimia 60 ya taka hizo zinaweza kurejelezwa ikiwa zitadhibitiwa vizuri kupitia uchumi rejeshi,"aliongeza.

"Kwa ngazi ya Kitaifa, Tanzania inakadiriwa kupoteza takribani hekta 469,420 za misitu kila mwaka kutokana na shughuli mbalimbali zisizo endelevu ikiwa ni pamoja na matumizi makubwa ya kuni na mkaa, kilimo kisicho endelevu, ufugaji holela pamoja na shughuli nyingine za kibinadamu zinazosababisha uharibifu wa mazingira hali inayochangia kuongezeka kwa gesi joto, kuharibu vyanzo vya maji na kuhatarisha usalama wa bioanuwai,".

Alieleza Upandaji wa miti yenye matumizi mbalimbali una mchango mkubwa katika kufyonza gesi ya kaboni, kupunguza mmomonyoko wa udongo, kuhifadhi vyanzo vya maji, kutoa matunda pamoja na kuongeza kipato kwa wananchi kupitia bishara ya Kaboni na kuongeza ustahimilivu dhidi ya athari za Mabadiliko ya Tabianchi.

"Matumizi ya nishati safi ya kupikia ni hatua muhimu katika kupunguza utegemezi wa kuni na mkaa ambao umeendelea kuwa miongoni mwa sababu kuu za uharibifu wa misitu nchini.

“Kuimarisha upatikanaji na matumizi ya nishati safi kama vile gesi asilia, umeme, biogas na teknolojia bora za kupikia kutasaidia kupunguza kasi ya ukataji miti, kupunguza uzalishaji wa gesi joto na kuboresha afya za wananchi hususan wanawake na watoto ambao huathirika zaidi na moshi unaotokana na matumizi ya nishati isiyosafi," alisisitiza.

Naye Mkuu wa Wilaya Arusha Mhe. Joseph Mkude alisema kila mmoja ana wajibu wa kutunza na kuhifadhi mazingira na kuzingatia matumizi ya nishati safi ya kupikia na kusema taasisi nyingi zinatekeleza agizo hilo.

Amesema arusha imekuwa ikifanya kila jitihada kuhakikisha jiji hilo linakuwa safi na kushirikisha jamii yote kutambua umuhimu wa utunzaji wa mazingira ndio maana wanafunzi wamepewa kipaumbele.



Na Mwandishi Wetu, Dodoma
SPIKA wa Bunge, Mussa Azan Zungu, ameibana Wizara ya Ujenzi akitaka mageuzi ya haraka katika utekelezaji wa miradi ya miundombinu kupitia mfumo wa Ubia kati ya Serikali na Sekta Binafsi (PPP), akionya kuwa kuendelea kutegemea serikali pekee kugharamia barabara ni mzigo mkubwa kwa taifa.

Katika msisitizo wake, Zungu alisema Tanzania haiwezi kufanikisha kikamilifu malengo ya maendeleo ya miundombinu bila kuipa nafasi sekta binafsi kushiriki katika uwekezaji wa barabara na miradi mingine mikubwa. Alieleza kuwa mataifa mengi duniani tayari yamepiga hatua kwa kutumia PPP kama suluhisho la changamoto za kifedha kwenye sekta ya miundombinu.

Amesema wakati umefika kwa Wizara ya Ujenzi kuacha kusita na kuonyesha dhamira ya kweli ya kuingia kwenye ubia huo, akibainisha kuwa mahitaji ya barabara nchini yanaendelea kuongezeka huku uwezo wa serikali kugharamia kila kitu ukiendelea kuwa finyu.

Zungu alikumbusha kuwa katika utekelezaji wa Vision 2050, sehemu kubwa ya miradi ya maendeleo  inayokadiriwa kufikia asilimia 70 — inatarajiwa kutekelezwa kwa kushirikisha sekta binafsi, jambo linalofanya mfumo wa PPP kuwa sehemu muhimu ya mkakati wa taifa wa maendeleo.

Akionyesha kutoridhishwa kwake na kasi ya wizara hiyo, Spika huyo alihoji mantiki ya serikali kuendelea kubeba mzigo mkubwa wa utekelezaji wa miundombinu peke yake wakati fursa ya kugawana gharama na majukumu ipo wazi kupitia sekta binafsi.

Kauli ya Zungu imekuja kama shinikizo jipya kwa Wizara ya Ujenzi kuharakisha mageuzi ya namna miradi ya miundombinu inavyotekelezwa, huku akisisitiza kuwa ubia wa PPP sasa ni lazima waonekane kama suluhisho la maendeleo badala ya chaguo la hiari.

Diwani wa Kata ya Ludete, Jumanne Misungwi, amepata chakula cha mchana na watoto waishio katika mazingira magumu,wanaozunguka katika Mamlaka ya Mji Mdogo wa Katoro.

Hafla hiyo ya chakula imefanyika jana wakati wa mkutano wa mwaka wa madereva bajaji katika mji huo.

Mbali na chakula hicho, madereva hao wa bajaji waliweza pia kutoa misaada ya mahitaji mbalimbali katika Kituo cha Watoto Wenye Mahitaji Maalumu cha Katoro Shule ya Msingi.

Akizungumza katika hafla hiyo, Diwani Misungwi amesema kuwa watoto hao wa mtaani ni sehemu ya jamii na wanapaswa kulindwa ili wajihisi bado jamii inawajali.

Amesisitiza kuwa kila mwanajamii ana wajibu wa kuhakikisha makundi yenye uhitaji yanapata faraja na msaada, badala ya kubaguliwa au kutelekezwa.

Katika siku hiyo muhimu ya waendesha bajaji, Misungwi amewapongeza vijana hao kwa kuandaa tukio hilo lenye kugusa maisha ya wengi.

Aliongeza kuwa kufanya matendo ya huruma na misaada kwa wenye uhitaji kutawawekea baraka katika shughuli zao za kila siku na kukuza mshikamano Katoro.




NA MWANDISHI WETU

TUME ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB) imewapongeza walimu wote kwa utekelezaji wa majuku yao kwa mujibu wa sheria na miongozo mbalimbali hususan kulinda haki za watoto na kupambana na ukatili dhidi ya watoto kuhakikisha wanakuwa katika mazingira bora.

Imesema watoto ni kundi ambalo linapaswa kulindwa, kukutetewa zaidi kwa sababu umri walio nao baadhi yao ni vigumu kujisemea, kujitetea au kujilinda dhidi ya ukatili mbalimbali unaoweza kufanywa na jamii inayowazunguka.

Hayo yameelezwa, na Ofisa Mfawidhi wa THBUB Tawi la Dar es Salaam, Shoma Ndono, katika hafla ya ufunguzi wa mafunzo kwa walimu walezi wa Klabu za Haki za Binadamu mkoani humo.

Shoma, amsemaTHBUB itaendelea kushirikiana kikamilifu na walimu walezi wa klabu hizo za haki za binadamu kuhakikisha zinakuwa imara na endelevu kwa faida ya jamii yote .

“Mafunzo haya yanahusu majukumu ya Tume za Haki za Binadamu na Utawala Bora na kupitia mwongozo wa uendeshaji wa klabu za haki za binadamu shuleni,”ameeleza Shoma.

Amebainisha pia yanalenga kuwawezesha walimu walezi wa klabu hizo kupata maarifa, stadi na mbinu za kulea wanafunzi wawe mabalozi wa haki, amani na utu.

“Mtoto anayejua haki zake anaweza kusimama na kuzitetea pamoja na kuheshimu hazi za wenzake. Pia watoto wafahamu kuwa THBUB ni chombo sahihi kuwasilisha malalamiko yao endapo itaonekana kuwa haiki zao ama za wengine zimevunjwa au zinakaribia kuvunjwa,”amesema ofisa huyo.

Shoma, amebainisha mafunzo hayo ni jukwaa muhimu la walimu walezi wa klabu za haki za binadamu kushirikishana uzoefu na changamoto mbalimbali wanazokabiliana nazo katika shughuli zao .

“Kupitia mafunzo haya tunatarajia kupata matokeo na mabadiliko makubwa hivyo kufikia lengo kwani THBUB inawawawezeshaji wazuri na mahiri wa kutoa mafunzo,”amesema.

Baadhi ya washiriki wa mafunzo hayo ambao ni walimu kutoka shule za msingi na sekondari mkoani Dar es Salaam, wameeleza mafunzo hayo yana umuhimu mkubwa kwao kwani watayafikisha kwa wanafunzi kupitia kalabu za haki.

Mwalimu wa Shule ya Msingi Umoja wa Mataifa, Ashura Kaisinika, ameishukuru THBUB kwa mafunzo hayo abayo yatamsaidia kuwasaidia watoto kufahamu haki zao, kujitetea hususan katika kipindi hiki ambapo vitendo vya ukatili vinaendelea kuchipua katika jamii.

“Mtoto atakuwa alozi mwema kwa jamii yake nay eye atakuwa kiongozi wa taifa baadaye hivyo kutambua haki zinazo stahili,”amesema Ashura.







Taasisi ya Saratani Ocean Road imeshiriki katika uzinduzi wa jukwaa la utoaji huduma za afya na bima zinazofanyika katika viwanja vya Posta-TTCL Kijitonyama.

Jukwaa hilo linalenga kuimarisha juhudi za serikali katika kuboresha afya kwa kutoa elimu ya afya kwa jamii.

Pia kuhamasisha kinga dhidi ya magonjwa mbalimbali pamoja na kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu umuhimu wa kujiunga na huduma za bima ya afya.

Taasisi ya saratani ocean road imepata fursa ya kutoa elimu ya saratani mbalimbali na kuwafanyia uchunguzi wa saratani ya matiti na saratani ya tezi dume kwa wananchi waliofika katika viwanja hivyo.

Aidha taasisi hiyo imewataka wananchi kufika katika viwanja hivyo kupata elimu na kuchunguzwa afya zao bila malipo yoyote.

Jukwaa hilo la utoaji huduma za afya na bima limeanza tarehe 20/05/2026 na linatarajia kumalizika tarehe 24/05/2026.



Na Janeth Raphael MichuziTv Bungeni Dodoma.

Serikali imeendelea kuimarisha mikakati ya kukabiliana na changamoto ya ajira kwa vijana nchini kwa kuanzisha na kusimamia programu mbalimbali zinazolenga kuwajengea uwezo wahitimu wa vyuo vikuu na vijana wengine ili waweze kuajirika au kujiajiri.

Hatua hizo zimeelezwa bungeni na Naibu Waziri wa Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Kazi, Ajira na Mahusiano, Dkt. Eveline Munisi, wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Amina Ali Mzee, aliyehoji hatua zinazochukuliwa na Serikali kupunguza tatizo la ajira kwa vijana wanaomaliza masomo yao.

Dkt. Munisi amesema Serikali imeandaa Mwongozo wa Taifa wa Mafunzo ya Uzoefu Kazini wa mwaka 2017, unaolenga kuratibu utoaji wa mafunzo kwa vitendo kwa kushirikisha sekta ya umma na binafsi ili kuwapa vijana nafasi ya kupata uzoefu wa kazi kabla ya kuingia rasmi kwenye soko la ajira.

Amesema kupitia mwongozo huo pamoja na Programu ya Taifa ya Kukuza Ujuzi inayosimamiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, vijana wengi wamepata mafunzo ya vitendo yanayowawezesha kuongeza ushindani katika soko la ajira.

Kwa mujibu wa Dkt. Munisi, jumla ya wahitimu 32,194 tayari wamenufaika na mafunzo hayo kwa kupata ujuzi wa kazi, maadili ya utumishi pamoja na uzoefu unaowasaidia kuajiriwa katika taasisi mbalimbali au kujiajiri katika maeneo yao.

Aidha, Serikali imeendelea kuanzisha programu maalum zinazowalenga vijana katika sekta zinazozalisha ajira kwa wingi ikiwemo kilimo kupitia programu ya Building a Better Tomorrow (BBT), sekta ya madini kupitia MBT pamoja na sekta ya uvuvi kupitia BBT-LIFE.

Dkt. Munisi amesema lengo la programu hizo ni kuwawezesha vijana kutumia fursa zilizopo katika rasilimali za nchi kwa kujenga uwezo wa uzalishaji, ubunifu na ujasiriamali ili waweze kujitegemea kiuchumi.

Katika hatua nyingine, Serikali imeendelea kufungua fursa za ajira nje ya nchi kwa kuwaunganisha Watanzania na waajiri wa kimataifa kupitia mikataba ya ushirikiano na mataifa mbalimbali ikiwemo Qatar, Saudi Arabia, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) pamoja na Iran.

Amesema katika kipindi cha Julai 2025 hadi Aprili 2026, jumla ya vijana 7,593 wamefanikiwa kupata ajira nje ya nchi kupitia mpango huo katika fani tofauti tofauti.

Serikali imeeleza kuwa itaendelea kuimarisha mazingira ya ajira na uwekezaji katika sekta mbalimbali ili kuhakikisha vijana wengi zaidi wanapata fursa za ajira na kushiriki kikamilifu katika kukuza uchumi wa taifa.


Na Janeth Raphael MichuziTv Bungeni Dodoma 

Mbunge wa Gairo, Ahmed Shabiby, amempongeza Afisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Vipimo Tanzania (WMA), Alban Kihulla, kwa utendaji wake wa kazi wenye weledi na ushirikiano mzuri katika kutekeleza majukumu ya taasisi hiyo.

Shabiby amesema WMA imekuwa ikitoa ushirikiano wa karibu kila inapohitajika, hali ambayo imechangia kuimarisha usimamizi wa vipimo na kulinda maslahi ya wananchi pamoja na wafanyabiashara nchini.

Mbunge huyo ametoa pongezi hizo leo Mei 22, 2026, Bungeni jijini Dodoma wakati akichangia hoja ya makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Viwanda na Biashara kwa mwaka wa fedha 2026/2027.

Pamoja na pongezi hizo, Shabiby ameishauri WMA kuongeza umakini katika kudhibiti ubora wa nondo zinazozalishwa na baadhi ya viwanda nchini, akieleza kuwa bado kuna changamoto ya uzalishaji wa nondo zisizokuwa na ujazo na viwango sahihi, jambo linaloweza kuhatarisha usalama wa majengo yanayojengwa kwa kutumia bidhaa hizo.

Amesema baadhi ya viwanda vinavyomilikiwa na wawekezaji wa kigeni vinaendelea kuzalisha bidhaa zenye viwango hafifu huku vikifanya biashara kama kawaida, hali inayohitaji hatua kali zaidi kutoka kwa mamlaka husika.

“Tusibaki kwenye kutoa faini pekee. Viwanda vinavyotengeneza nondo zisizokidhi viwango vinapaswa kufungiwa ili kulinda usalama wa wananchi na ubora wa ujenzi nchini,” amesema Shabiby.

Aidha, amesisitiza kuwa usimamizi madhubuti wa viwango vya bidhaa za ujenzi ni muhimu kwa maendeleo ya sekta ya viwanda pamoja na kulinda maisha na mali za Watanzania.



Na Janeth Raphael MichuziTv Bungeni Dodoma .

Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) imeweka mikakati kabambe ya kuimarisha utendaji wa Mfumo wa Stakabadhi za Ghala katika mwaka wa fedha 2026/2027, ikiwa ni sehemu ya juhudi za Serikali kuongeza ufanisi wa biashara ya mazao na kuhakikisha ubora wa bidhaa zinazohifadhiwa nchini.

Akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Viwanda na Biashara bungeni, Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga, amesema WRRB imejipanga kuboresha usimamizi wa mfumo huo ili uweze kufanya kazi kwa viwango vya juu zaidi na kuwanufaisha wakulima pamoja na wafanyabiashara.

Amesema miongoni mwa hatua zitakazotekelezwa ni kuimarisha udhibiti wa ubora wa mazao yanayoingia na kutoka kwenye maghala yaliyo chini ya mfumo huo, sambamba na kuongeza ufuatiliaji kwa waendesha maghala, wakaguzi na mameneja dhamana ili kuhakikisha uwajibikaji na uzingatiaji wa sheria na kanuni zilizowekwa.

Aidha, WRRB itaendelea kutoa elimu kwa umma na kufanya kampeni za uhamasishaji kuhusu matumizi ya Mfumo wa Stakabadhi za Ghala, hatua inayolenga kuongeza uelewa kwa wakulima na wafanyabiashara kuhusu faida za mfumo huo katika uhifadhi salama na uuzaji wa mazao kwa tija zaidi.

“WRRB imejipanga kuendeleza kampeni za elimu kwa umma na kuongeza uhamasishaji kuhusu matumizi ya Mfumo wa Stakabadhi za Ghala ili kuongeza ushiriki wa wadau mbalimbali,” amesema Kapinga.

Katika hatua nyingine, Bodi hiyo inaendelea na mchakato wa kupata cheti cha ithibati ya ubora wa kimataifa (ISO), hatua inayotarajiwa kuongeza uaminifu wa mfumo huo ndani na nje ya nchi pamoja na kuongeza ushindani katika masoko ya kikanda na kimataifa.

Serikali inaamini kuwa maboresho hayo yatachangia kuongeza thamani ya mazao ya wakulima, kupunguza upotevu wa mazao baada ya mavuno na kuongeza mapato kwa wananchi pamoja na kukuza uchumi wa taifa.

WRRB imeeleza kuwa utekelezaji wa mipango hiyo ni sehemu ya mkakati wa muda mrefu wa kuifanya sekta ya kilimo kuwa na tija kupitia matumizi ya mifumo ya kisasa ya uhifadhi, usimamizi na biashara ya mazao nchini.




Na Janeth Raphael MichuziTv Bungeni Dodoma.

Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga, ameomba Bunge kuidhinisha jumla ya shilingi 137,812,633,000 kwa ajili ya utekelezaji wa majukumu ya Wizara hiyo katika mwaka wa fedha 2026/2027, ikiwa ni sehemu ya jitihada za Serikali kuendelea kukuza uchumi wa viwanda na kuimarisha mazingira ya biashara nchini.

Waziri Kapinga ameyasema hayo leo bungeni wakati akiwasilisha hotuba ya makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Viwanda na Biashara kwa mwaka wa fedha 2026/2027, akieleza kuwa fedha hizo zitasaidia kuendeleza mipango mbalimbali ya maendeleo ya sekta ya viwanda, biashara, uwekezaji pamoja na kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania katika soko la ndani na nje ya nchi.

Amesema kati ya fedha zinazoombwa, shilingi 104,122,530,000 ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida ya Wizara, huku shilingi 33,690,103,000 zikitengwa kwa matumizi ya maendeleo yanayolenga kuimarisha miradi na shughuli mbalimbali za kimkakati ndani ya sekta hiyo.

Akifafanua zaidi kuhusu matumizi ya kawaida, Waziri Kapinga amesema jumla ya shilingi 78,049,345,000 zitatumika kulipa mishahara ya watumishi wa Wizara na taasisi zake, huku shilingi 26,073,185,000 zikielekezwa kwenye matumizi mengineyo ikiwemo uendeshaji wa shughuli za kila siku, usimamizi wa programu mbalimbali pamoja na utekelezaji wa majukumu ya Wizara katika maeneo tofauti nchini.

Kwa upande wa bajeti ya maendeleo, Waziri huyo amesema fedha zote za maendeleo zinazotarajiwa kutumika katika mwaka huo wa fedha ni fedha za ndani, jambo alilosema linaonesha dhamira ya Serikali ya kujitegemea katika kugharamia miradi ya maendeleo na kuendelea kuimarisha uchumi wa taifa kupitia sekta ya viwanda na biashara.

Aidha, Waziri Kapinga amesema Wizara itaendelea kusimamia utekelezaji wa sera na mikakati mbalimbali inayolenga kuongeza uzalishaji wa viwandani, kuvutia uwekezaji, kuongeza thamani ya mazao na bidhaa zinazozalishwa nchini pamoja na kufungua fursa zaidi za ajira kwa wananchi, hususan vijana.

Katika hotuba yake, Waziri huyo pia alisisitiza umuhimu wa sekta binafsi kushirikiana na Serikali katika kufanikisha agenda ya maendeleo ya viwanda nchini, akibainisha kuwa mazingira bora ya biashara yanaendelea kuboreshwa ili kuwavutia wawekezaji wa ndani na nje ya nchi.

Sambamba na hilo, amesema Serikali itaendelea kuimarisha mifumo ya biashara, kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania katika masoko ya kimataifa na kuhakikisha viwanda vya ndani vinapata mazingira rafiki ya uzalishaji na biashara.

Waziri Kapinga ameongeza kuwa wananchi na wadau mbalimbali wanaweza kupata hotuba hiyo kwa undani zaidi kupitia tovuti rasmi ya Wizara ya Viwanda na Biashara.


NA FARIDA MANGUBE MOROGORO

Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kimeandika rekodi ya kipekee nchini baada ya kutangaza kufanikiwa kupata Hati Safi kutoka kwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa miaka 20 mfululizo.

Rekodi hiyo ya kihistoria ya uwajibikaji na usimamizi bora wa fedha imetangazwa wakati wa Mahafali ya 47 ya chuo hicho yaliyofanyika katika Kampasi Kuu ya Edward Moringe.

Mbali na rekodi hiyo ya CAG, SUA imeendeleza ubabe wake wa kifedha baada ya kutunukiwa tuzo ya kuwa taasisi ya juu ya elimu inayoongoza kwa uandaaji bora wa hesabu nchini na Bodi ya NBAA kwa miaka mitatu mfululizo.

Mafanikio haya makubwa yameongeza chachu ya furaha katika mahafali hayo yaliyoshuhudia jumla ya wahitimu 877 wakitunukiwa shahada za Uzamivu, Uzamili, Shahada za Kwanza, Stashahada za juu, Stashahada na Astashahada mbalimbali chini ya uongozi wa Mkuu wa Chuo, Jaji Joseph Sinde Warioba.

Akiwasilisha ripoti hiyo ya mafanikio ya fedha na utawala bora mbele ya hadhara, Makamu Mkuu wa Chuo, Profesa Raphael Chibunda amesema

"Tumendelea kuimarisha nidhamu katika majukumu ya chuo, na hatua hiyo imekiwezesha chuo chetu kupata hati safi kutoka kwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG). Hii inaendeleza rekodi yetu ya hati safi kwa dhihirisho la miaka 20 mfululizo."

Profesa Chibunda amebainisha kuwa wahitimu hao 877 wanatoka katika programu 83 za masomo kati yao, wanaume ni 517 na wanawake ni 360.

Uchambuzi wa kitaaluma unaonyesha kuwa wahitimu wa Shahada za Kwanza (Bachelor) walikuwa 698, Shahada za Umahiri (Masters) 132, Shahada za Uzamivu 19, Stashahada 141, na Astashahada 23.

Katika hatua nyingine ya maendeleo, Profesa Chibunda ametangaza kuwa chuo kipo hatua za mwisho kuzindua kituo chake rasmi cha runinga cha SUA TV, ambacho kitakuwa nyanja ya kimkakati ya kusambaza teknolojia za kisasa za kilimo, mifugo, na uvuvi kwa jamii.

Pia, amejivunia vijana wa SUA Innovation Hub kupitia timu za Snackers Square na Eco Mushroom kwa kushika nafasi ya kwanza kitaifa kwenye mashindano ya Youth Ignite Student Founders Fellowship, akisisitiza kuwa chuo kimebobea katika kuwajenga wanafunzi kiuandishi na kiubunifu.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Baraza la Chuo, Ndugu Andrew Masawe, akizungumza kuhusu dira na majukumu ya Baraza katika kusimamia chuo, ameeleza kuwa Baraza limeendelea kuboresha sura na utendaji wa Chuo kwa ujumla.

"Baraza limeendelea kwa kiasi kikubwa kutekeleza mambo mengi makubwa yanayolenga kuboresha sura na utendaji wa chuo kwa ujumla Pia, Baraza limeidhinisha nyaraka muhimu za kimkakati ikiwemo miongozo ya ukuzaji wa machapisho ya Maktaba ya Taifa ya Kilimo ya mwaka 2025."Amesema Massawe.

Masawe ametaja pia kuanzishwa kwa Kituo kipya cha Sera na Mafunzo ya Kimkakati (SUA Center for Policy and Strategic Studies) ili kuishauri serikali katika sera zenye tija, huku akitoa shukrani za dhati kwa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa shilingi bilioni 20.7 kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya Kampasi ya Mizengo Pinda mkoani Katavi.





WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete, leo ameshiriki ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa 13 wa Chama cha Waandishi Waendesha Ofisi Tanzania (TAPSEA) uliofanyika katika ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano wa Ngurdoto, mkoani Arusha.

Mkutano huo umefunguliwa rasmi na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, na umewakutanisha zaidi ya wanachama 5,050 wa TAPSEA kutoka Serikali Kuu, Serikali za Mitaa, taasisi mbalimbali za umma pamoja na wajumbe kutoka Tanzania Bara na Zanzibar.

Akizungumza wakati wa ufunguzi huo, Makamu wa Rais Dkt. Nchimbi aliwataka wajumbe wa mkutano huo, ambao pia unatarajiwa kuchagua viongozi wapya wa chama hicho, kuzingatia haki, mshikamano na maslahi ya taasisi yao, huku akisisitiza umuhimu wa kuepuka migogoro na mambo yanayoweza kukipotezea mwelekeo chama hicho muhimu kwa maendeleo ya utumishi wa umma nchini.

Kwa upande wake, Mhe. Ridhiwani Kikwete, akizungumza kabla ya kumkaribisha mgeni rasmi, aliwakumbusha wajumbe hao juu ya juhudi kubwa zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuboresha ustawi wa watumishi wa umma nchini.

Alieleza kuwa Serikali imeendelea kupandisha madaraja watumishi, kuboresha miundo na vyeo vya kazi, pamoja na kulipa madeni mbalimbali ya mishahara na stahiki za watumishi, huku akiahidi kuwa juhudi hizo zitaendelea kadri hali ya bajeti ya Serikali itakavyoruhusu.

“Tumekuwa tukifanya maboresho haya hatua kwa hatua, na dhamira yetu ni kuhakikisha watumishi wa umma wanaendelea kunufaika na matunda ya Serikali yao,” alisema Mhe. Ridhiwani.

Mkutano huo wa TAPSEA unatarajiwa kujadili masuala mbalimbali yanayohusu maendeleo ya taaluma ya uandishi na uendesha ofisi pamoja na mustakabali wa chama hicho nchini.



Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Dodoma, Neema Peter Majule, ameibana Serikali akiitaka kueleza mkakati wake wa kuwasaidia wahitimu wa vyuo vikuu kutumia vyeti vyao vya taaluma kama dhamana ya kupata mikopo kwa ajili ya kuanzisha biashara na miradi ya uwekezaji.

Akizungumza bungeni Jijini Dodoma Mei 21, wakati akiuliza swali namba 409 kwa Wizara ya Fedha, Dkt. Majule alisema kuwa sera ya elimu ya juu kwa sasa inalenga kuzalisha wahitimu wanaoweza kujiajiri na pia kuajiri wengine kupitia miradi mbalimbali ya maendeleo. 

Alieleza kuwa vyuo vikuu vingi Duniani vimeanzisha idara za Career Development kwa lengo la kuwaandaa vijana hao kuingia kwenye ulimwengu wa biashara na uwekezaji mkubwa.

Katika swali lake la kwanza, Dkt. Majule alihoji kama Serikali ipo tayari kuwabaini wahitimu wenye ubunifu na uwezo wa kuanzisha miradi mikubwa, na kuwapatia mikopo mikubwa ili waweze kufungua biashara zitakazosaidia kutoa ajira kwa Watanzania wengine.

Aidha katika swali lake la pili, mbunge huyo alihoji kama Serikali ipo tayari kutoa mitaji mikubwa kwa wahitimu watakaotumia vyeti vyao vya taaluma kama dhamana ya mikopo, au kama bado watahitajika kuwa na dhamana nyingine za ziada ili kupata fedha hizo.

Akijibu maswali hayo, Naibu Waziri wa Fedha Mhe. Laurent Luswetula, amesema Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan inaendelea kuweka mazingira rafiki ya kuwawezesha vijana kiuchumi kupitia programu mbalimbali ya mikopo yenye masharti nafuu, na tayari Serikali imetoa mabilioni ya fedha kwa ajili ya kuwawezesha vijana kujiajiri na kuanzisha shughuli za kiuchumi.

Hata hivyo, ameeleza kuwa changamoto kubwa iliyopo ni kwamba wahitimu wengi wa vyuo vikuu bado hawana uzoefu wa kutosha katika kuendesha biashara kubwa na uwekezaji wa kiwango kikubwa. 

Amesema Serikali inaamini vijana wanapaswa kuanza na biashara ndogo huku wakijengewa uwezo wa ujasiriamali, usimamizi wa biashara na uwekezaji kabla ya kufikia hatua ya kupata mikopo mikubwa.






📍Njombe

Mradi mkubwa wa uzalishaji wa kokoto uliopo mtaa wa Kambarage kata ya Njombe Mjini, unatarajiwa kuongeza upatikanaji wa kokoto na kuchochea shughuli za kiuchumi na kuongeza mapato ya Serikali katika Mkoa wa Njombe.

Mradi huo unaomilikiwa na mchimbaji mdogo wa madini ya ujenzi, Isaya Boniface, umefungwa mtambo mkubwa wa kusaga kokoto wenye uwezo wa kuzalisha zaidi ya tani 1,000 kwa siku kwa kushirikiana na kampuni ya India ya Shree Sonal Earth Ltd iliyotoa usaidizi wa kitaalam katika utekelezaji wake.

Akizungumza kuhusu mradi huo, Boniface amesema uwekezaji huo utamaliza changamoto ya upatikanaji wa kokoto ambazo kwa muda mrefu zimekuwa zikisafirishwa kutoka mikoa ya Iringa, Dodoma na Pwani, hususan Lugoba, kwa matumizi ya miradi mbalimbali ya ujenzi mkoani Njombe.

Amesema mradi huo utasaidia kupunguza gharama za ujenzi, kuongeza ajira kwa wananchi, kukuza mzunguko wa fedha pamoja na kuimarisha utekelezaji wa miradi ya maendeleo inayohitaji kokoto kwa kiwango kikubwa.

Kwa upande wake, Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Njombe, Mhandisi Lucas Mlekwa, amesema mradi huo ni miongoni mwa uwekezaji muhimu unaotarajiwa kuongeza mapato ya Serikali kupitia madini ujenzi.

Amesema kutokana na uwezo wa uzalishaji wa tani 1,000 za kokoto kwa siku, Serikali inatarajia kukusanya zaidi ya shilingi milioni 2.3 kwa siku kupitia tozo za mrahaba na ada ya ukaguzi, huku makadirio ya mapato ya mwaka yakifikia kati ya shilingi milioni 400 hadi 600.

“Mkoa wa Njombe unaendelea kushuhudia ukuaji mkubwa wa sekta ya ujenzi wa miundombinu, makazi na miradi ya Serikali, hivyo uwepo wa mradi huu utaongeza upatikanaji wa malighafi muhimu kwa utekelezaji wa miradi hiyo,” amesema Mhandisi Mlekwa.

Aidha, amesema Serikali chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuweka mazingira rafiki kwa wachimbaji wadogo kwa kushirikiana na taasisi za kifedha ili kuwawezesha kupata mikopo na vifaa vya uzalishaji.

Mhandisi Mlekwa ameongeza kuwa miradi mikubwa ya maendeleo inayotekelezwa mkoani Njombe, ikiwemo mradi wa kiwanda cha chuma, itaongeza mahitaji ya kokoto na kufungua zaidi fursa za uwekezaji katika sekta ya madini ya ujenzi.








NA FARIDA MANGUBE, MOROGORO 

Katika kipindi hiki cha kasi ya maendeleo ya teknolojia na mabadiliko makubwa ya mifumo ya mawasiliano duniani, waandishi wa habari hususan wanawake wametakiwa kuongeza juhudi katika kujiendeleza kielimu na kujikita kwenye taaluma za ubobezi ili kuendana na ushindani wa sekta ya habari na kuchangia maendeleo ya jamii.

Wito huo umetolewa mkoani Morogoro wakati wa Mahafali ya 47 ya Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), ambapo baadhi ya wahitimu wa fani mbalimbali, akiwemo mwanahabari Kelvin Gwabala na Sophia Makame, walizungumza kuhusu umuhimu wa wanahabari kuendelea kujifunza na kuongeza ujuzi wa kitaaluma.

Akizungumza mara baada ya kuhitimu, Kelvin Gwabala amesema maendeleo ya teknolojia yamebadilisha mfumo wa utoaji habari, hivyo wanahabari wanapaswa kujifunza mbinu mpya za uandishi na matumizi ya teknolojia ili kubaki na ushindani katika tasnia hiyo.

Kwa upande wake, Sophia Makame amesisitiza umuhimu wa wanawake waliopo kwenye sekta ya habari kujiamini na kutumia fursa za elimu kujijengea uwezo wa kitaaluma, akieleza kuwa elimu ndiyo msingi wa mafanikio katika kazi za habari.

Profesa Raphael Chibunda ni Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA),  amesema chuo hicho kinaendelea kuboresha mazingira ya kujifunzia pamoja na kuongeza programu mbalimbali zinazolenga kuwaandaa wahitimu wenye uwezo wa kukabiliana na mahitaji ya soko la ajira la sasa.

Aidha, Mwenyekiti wa Baraza la Chuo hicho, Andrew Massawe, amesema SUA imeendelea kupata mafanikio katika sekta za elimu, utafiti na ubunifu, huku akibainisha kuwa chuo hicho kitaendelea kuwekeza katika kukuza taaluma zinazochochea maendeleo ya taifa.







Top News