washa(kulia)==================================
Na Tiganya Vincent-MAELEZO-Dodoma
Serikali imeanza mchakato wa kukusanya maoni ya wananchi mbalimbali kwa ajili maandalizi ya uzinduzi wa mkakati wa kukuza uchumi Tanzania (MKUKUTA) awamu ya pili ambao unatarajiwa kuanza kutekelezwa hapa kuanzia Julai Mosi mwaka huu.
Waziri wa Fedha na Uchumi Mustapha Mkulo alisema awamu hiyo ya pili inakuja baada ya kuonekana kwa mafanikio katika awamu ya kwanza ambayo ni pamoja na kukua na kuimarika kwa uchumi, kuboreka kwa upatikanaji wa huduma za jamii, kuboreka kwa elimu na kupungua kwa vifo vya watoto wachanga.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Dodoma jana Mkulo alisema kuwa mbali na mafanikio hayo bado zipo changamoto zilizojitokeza katika awamu ya kwanza ya MKUKUTA ambazo zinaendelea kufanyiwa kazi ikiwemo mazingira magumu ya biashara, uzalishaji duni katika kilimo, upungufu wa mikopo ya kilimo, uzalishaji nishati usioridhisha na udhaifu wa miundombinu.
Waziri huyo wa Fedha alisema katika awamu ya pili Serikali imejipanga kutatua changamoto zilizopo na kuonyesha mafanikio zaidi kwa kulenga sekta zinazochangia kwa kiasi kikubwa katika pato la Taifa ikiwemo Sekta ya Utalii, Madini, Uzalishaji wa mazao ya kilimo na kuwekeza katika miundombinu ya biashara.
Alisema kuwa katika MKUKUTA II , Serikali imetilia mkazo katika kilimo kupitia uwekezaji ili kuinua uzalishaji wa mashambani na hivyo kutoa maisha bora kwa wananchi wa vijijini na kuongeza kuwa uwekezaji katika sekta ya kilimo utakwenda sanjari na kauli mbiu ya kilimo kwanza.
Mkulo aliongeza kuwa eneo jingine lilopewa kipaumbe katika awamu ya pili ya MKUKUTA ni upanuzi na uboreshaji viwanda ili kuongeza wigo wa ajira kwa wananchi na kuwasaidia wajasirimali kuweza kujimudu.
Vile vile waziri Mkulo alisema kuwa uwekezaji katika miundombinu umepewa kipaumbele kwa ajili ya kusaidia kujenga uchumi shindanishi na ukuzaji wa uchumi kwa ujumla.
Kwa upande wa sekta ya utalii , awamu ya pili ya MKUKUTA inakusudia kujenga uwezo wa wataalamu wa sekta hivyo , kujenga miundombinu ya kuvutia watalii wengi zaidi na kuimarisha ushirikiano wa sekta ya utalii na nyingine ili isaidie kunuia uchumi wan chi haraka.
Aidha Mkulo aliongeza kuwa Serikali imekusudia kuongeza viwanda vya kuongeza thamani ya madini na kuwawezesha wachimbaji wadogo wadogo ili wapate vifaa muhimu vya uchimbaji madini.
Katika hatua nyingine Serikali imeamua kupunguza bei ya ushuru wa soko kwa mazao ili kuwawezesha wakulima kunufaika na kilimo wanachokiendesha badala ya kutumia fedha nyingi katika kilipia kodi.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Uchumi upande wa Huduma Bwana John Haule amesema kodi hizo zitaendelea kupunguzwa kila mwaka lengo likiwa ni kuziondoa kabisa ili kumpatia nafuu mkulima.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Dodoma Haule amesema sanjari na kupunguzwa kwa kodi hizo Serikali imeamua kuingiza katika mfumo wake wa mapato, mapato ya Halmashauri lengo likiwa ni kutaka kujua vyanzo vya mapato vya Halmashauri na uhalali wake.
Amebainisha kuwa Halmashauri zimeagizwa kushirikiana na Mamlaka za Mapato (TRA), katika kubadilishana ujuzi ili ziweze kuwa na vyanzo vingi zaidi vya mapato ambavyo havitategemea kodi kutoka kwa wananchi.


kwa vifupisho tu watanzania ni 100%bora zaidi.
ReplyDeletekwa utendaji na utekelezaji ni uozo0.000%
rushwa tu!!
Tunashukuru angalau taifa limepata habari za uwepo wa MKUKUTA mwingine. Kuna njia ya diaspora kutoa maoni kupitia mtandao au ndio tulie tu? Vipi na ule 'MKURAMBITA'?
ReplyDelete