KESI inayomkabili Waziri wa zamani wa Wizara ya Fedha, Basil Mramba, aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini Daniel Yona na Katibu Mkuu wa zamani wa Fedha, Grey Mgonja, imeendelea leo katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam, ambapo shahidi upande wa mashitaka Godwin Nyelo amegoma kutoa barua iliyokuwa ikitoka Benki kuu ya Tanzania (BOT) kwenda kampuni ya M/S Alex Stewart Government Business Cooperation kama kielelezo cha ushahidi kwa upande wa utetezi mahakamani kwa kuwa sio yake.
Barua hiyo inadaiwa kuandikwa na aliyekuwa msaidizi wa Gavana wa BoT, Daudi Balali, Kesia Mbatia Novemba 28, 2002 akiialika kampuni ya Alex Stewart kuwasilisha mchanganuo (proposal) ambao ulipelekea kuingiwa kwa mkataba kati ya BOT na kampuni hiyo
Hakimu Saul Kinemela aliyekuwa akisikiliza kesi hiyo alisema ili kutenda haki Mahakama inamlazimisha shahidi kutoa barua hiyo kama kielelezo cha ushahidi kwa upande wa utetezi.
Akitoa ushahidi wake mbele ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu shahidi huyo amedai kuwa anaikumbuka barua hiyo, lakini hawezi kuiongelea wala kuitoa kama kielelezo cha ushahidi kwa upande wa utetezi mahakamani hapo kwa sababu siyo yake na wala taasisi iliyohusika yeye hakuwa anaifanyia kazi.
Katika kesi hiyo, mawaziri hao wa zamani kwa pamoja wanatuhumiwa kuingia mkataba na kuisamehe kodi kinyume cha sheria kampuni ya Alex Stewart jambo linalodaiwa kuwa lilisababisha Serikali kupata hasara ya Sh bilioni 11.
Washtakiwa hao wanadaiwa kutenda makosa hayo kwa nyakati tofauti kati ya Agosti mwaka 2002 na Juni 14 mwaka 2004.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...