Naibu Waziri wa  Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mhe. Mahadhi Juma Maalim (MB) akizungumza wakati wa Mkutano wa  16 wa Mawaziri wa  Mambo ya Nchi za Nje wa nchi  Zisizofungamana na Upande Wowote ( Non-Aligned Movement) NAM.  Mkutano huo uliowakutanisha mawaziri na ma-naibu mawaziri kutoka nchi 120, umefanyika Bali, Indonesia na kumalizika mwishoni mwa wiki. Pamoja na mambo mengine, Mawaziri hao wameitaka Israel kuwaachia wafungwa wa kisiasa wa Kipalestina ambao miongoni mwao ni watoto chini ya miaka 18 na wanawake. Pamoja na kutaka kuwapo kwa mataifa mawili ya wapalestina na waisrael wakiishi   sambamba kwa kuzingatia mipaka ya mwaka 1967.

Na Mwandishi Maalum, New York

Mawaziri wa Mambo ya Nje  kutoka  nchi zisizofungamana na upande wowote   maarufu kama Non –Aligned Movement (NAM), wameitaka Israel kuwaachia huru wafungwa wa  kisiasa wa  Kipalestina.

Mawaziri hao ambao walikutana kwa siku nne katika mkutano wao wa 16 uliofanyika Bali, nchini Indonesia, wamesisitiza katika tamko lao kwamba   kitendo cha   Israel kuwaachia wafungwa  hao kitakuwa nikupiga  hatua moja muhimu kuelekea mchakato wa  amani ya kudumu.

Ujumbe wa Tanzania katika mkutano huo umeongozwa na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje  na  Ushirikiano wa Kimataifa Mhe. Mahadhi Juma Maalim (MB). Balozi wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, Mhe. Ombeni Sefue alikuwa miongoni mwa wajumbe wa Tanzania katika  mkutano huo.

Mawaziri hao  katika tamko lao wameitaka  Israeli kuachia huru idadi kubwa ya wafungwa wa kisiasa  wa kipalestiana, kitendo ambacho kitatafisiriwa kama hatua sahihi inayolenga kujenga mazingira ya kuaminiana  na kufungua milango ya mazungumzo kati ya  pande hizo mbili zinazohasimiana.

“Tunaitaka Israeli kuwaachia huru angalau wafungwa 300 ambao kati yao ni watoto walio chini ya miaka 18 wakiwamo pia wanawake. Tunasikitishwa sana na mwendelezo wa vitendo visivyo vya kibinadamu dhidi ya wapalestina” inasema sehemu  ya tamko hiko.

Inakadiriwa kwamba kuna wafungwa  wa kiasiasa wa Kipalestina wapatao 6,000 waliofungwa  nchini Israel.

Kupitia tamko hilo, Mawaziri wa NAM wanasema  licha ya kuitaka Israel kuwaachia huru wafungwa hao wa kisiasa, pia inaunga mkono  uwepo wa mataifa mawili yanayoishi sambamba kwa  kuzingatia mipaka ya  mwaka 1967.

Akizungumza wakati wa mkutano huo Naibu Waziri Mahadhi Juma Maalim, amesema, wakati Tanzania  ikiridhishwa  na  kile ambacho NAM imefanikiwa  kukitekeleza katika kipindi cha miaka 50 tangu kuanzishwa kwake, lakini bado inasikitishwa sana na kutopatikana kwa ufumbuzi wa suala zima la  matatizo ya Palestina.

  Tatizo la Palestina limesuasua kwa muda murefu sana, na kusababisha madhara makubwa. Ujumbe  wa Tanzania leo hii  ni  mfupi na ulio wazi,  nao ni kwamba, madhara na maumivu wanayoyapata wananchi wa palestina ni lazima  sasa yakomeshwe ” anasema  Naibu Waziri

Na kuongeza. “ Maeneo yanayokaliwa kimabavu na waisraeli lazima yarudishwe kwa wananchi wa Palestina. Na  ndoto iliyodumu kwa muda mrefu ya  wananchi wa  Palestina  ya kuwa na taifa lao huru na mji mkuu wao ukiwa ni  Mashariki ya Jerusalemu, wakiishi sambambana na kwa amani na usalama na taifa la  Israeli ni lazima itimie  sasa”.

Akabainisha kwamba,   Jumuia ya Kimataifa inaowajibu wa kutowaangusha wananchi wa Palestina,  halikadhalika NAM nayo haipashwi kuwaangusha  raia wa Palestina.

Akizungumzia wajibu wa NAM na hasa katika kipindi hiki ambacho dunia inakabiliwa na changamoto  mbalimbali, Naibu Waziri anasema  wanachama wa NAM wanatakiwa kuwa kitu kimoja na kushikamana wakati huu kuliko wakati mwingine wowote.

Anasema  Naibu Waziri , nchi wanachama wa  NAM ambazo hivi sasa wamefikia 120 baada ya kujiunga kwa FIJI na AZEBAIJAN wanatakiwa kushikamana na kuwa kitu kimoja katika kuzikabili changamoto za sasa na zile  mpya zitakazoimbuka.

“ Ni lazima na ni wajibu wetu kutumia nguvu na uwingi wetu, tupo wanachama 120 hivi sasa, idadi hii inatupa nguvu  ya kusukuma mbele  ajenda  zinazolenga  kuleta mabadiliko katika mfumo wa utendaji kazi wa Umoja wa Mataifa na taasisi nyingine za kimataifa.” akasema

 Na kuongeza kuwa  idadi ya wanachama wa NAM inawawezesha    kuitisha mabadiliko katika utekelezaji wa ahadi za mipango ya maendeleo, kusisitiza upokonyaji wa silaha,  uwepo wa  mifumo  halali na sawa ya biashara  na itakayojielekeza katika uainishaji wa matakwa sahihi ya nchi maskini zaidi duniani.

“haya ni mambo ambayo tunaweza kuyasimamia kama tukiamua.” Anasema Naibu Waziri.

Akimnukuu Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere kuhusu nguvu na wajibu wa   NAM katika masuala mbalimbali yakiwamo ya nguvu za kiuchumi.



Alisema hivi  miaka ya 1970 na hapa ninamnukuu “ Tunaweza kusaidiana kuimarisha uhuru wetu na kukataa kutaliwa kiuchumi kwa kufanya kazi kwa pamoja na kushirikiana kwa faida yetu pamoja. Kwa sababu hatutaweza kamwe kuwa  na uhuru wa kweli  kama tu wadhaifu kiuchumi, huku matarajio yetu kiuchumi  yakitulazimsiha kupiga makoti kama vile waokotezaji au  ombaomba kutoka kwa mataifa makubwa”.



Mkutano huo wa 16 wa Mawaziri wa Mambo ya Nje wa NAM licha  ya kujadili suala la Palestina, pia walijadiliana kwa kina na kubadilishana  mawazo kuhusu mwelekeo  na mchango wa  baadaye wa  NAM katika kipindi cha miaka 50 ijayo na hasa kwa kuzingiatia  mabadiliko makubwa na changamoto mbalimbali zinazoikabili dunia hivi sasa.

NAM ambayo imetimiza miaka 50 tangu kuanzishwa kwake mwaka 1961 pamoja na kutoa mchango mkubwa sana katika kipindi cha uhai wake,  yakiwamo mafanikio ya kumalizwa kwa ukoloni.

Lakini baada ya kumalizika kwa  vita baridi ambayo  hasa ndiyo iliyopeleka kuanzishwa kwa  chombo hicho kisichofungamana na upande wowote. Sasa  NAM inalazimika kujitazama upya na kutafakari nafasi yake, nguvu yake na ushawishi wake katika dunia inayobadilika kwa kasi huku ikikabiliwa na changamoto  mbalimbali.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

Kuna Maoni 6 mpaka sasa

  1. AnonymousMay 28, 2011

    Israel haiwezi kutakiwa na Tanzania kuachia wafungwa wa Palestina, baadhi ya watu walifungwa si kwa sababu ya kisiasa bali masuala ya kiusalama zaidi, Israel ni lazima ijilinde kutokana na maneno ya majirani zake kutaka kuiangamiza, nashauri Tanzania tusiingie sana kwenye suala ya Israel na Palestina kwa sababu si tu kwamba our opinion will not count, but all the nature of the conflict. Israel haiwezi kuweka usalama wake rehani kwa sababu tu jumuiya ya kimataifa inawataka kuwaachia wafungwa. Jerusalem itabaki kuwa mji mkuu wa Israel na kamwe haitagawanywa so we should just accept and move on.

    ReplyDelete
  2. AnonymousMay 28, 2011

    sihisi kama hili tamko linawakilisha mawazo na imani za watanzania wengi, hasa wakristo.

    biblia imeandikwa kuwa Mungu alimwambia Israeli "nitambariki atakayekubariki na ntamlaani atakayekulaani"

    sidhani kama wakristo wako radhi kukubali nchi ya ahadi igawiwe

    hotuba kama hizi ziko awamu hii ya nne tuu.

    ReplyDelete
  3. AnonymousMay 28, 2011

    niko radhi kulaaniwa kuliko kushangilia manyanyaso na mauwaji kwa ajili ya kipande cha ardhi.

    ReplyDelete
  4. AnonymousMay 28, 2011

    Wewe mdau unaetaka kuleta udini hapa, kwanini Nyerere alilitambua taifa la Palestina, kwani yeye si Mkristo?

    Issue ya Palestina na Israel ni ya muda mrefu lakini mimi niwaulize bila ya kuweka dini yo yote mbele. Hivi akija muafrika akakwambia hii ardhi ilikuwa yangu miaka elfu mbili nyumba uondoke haraka au akuondoshe kwa nguvu, wewe utatulia tu na kusema asante bwana?

    Ni ukweli usiopingika kwamba Israel wanaiba ardhi ya watu upande wa Egypt, Syria na hiyo Palestina, jee hao watulie tu? Mbona nyinyi kipande cha ardhi ya Tanzania kilipomegwa na Idi Amin hamukutulia na kusema asante?

    ReplyDelete
  5. AnonymousMay 28, 2011

    Achani hisia za kidini nyinyi narrow minded squirels, ina maana gani kusema 'eti awamu ya nne .....'. Na ina maana sasa Judaism na Christianity ni dini moja? Someni ili muepukane na ujinga.

    ReplyDelete
  6. AnonymousMay 29, 2011

    nyie washangilien MAANA HAMJUI CHOCHOTE lakin sik zao ziko karibun maana walikuwa wanalindwa sana na vibaraka wa kiarab na hao sasa wanatolewa mpaka(BORDER) ndo umeshafunguliwa kat ya gaza na egypt wataipata fresh na kama si WAmarekan kuwasaidia wasingekuwepo madhalim maana nyie mnaongea wana mpaka chakula chao huku europe ukugusa na kitu kingine hawanunui walivyo WABINAFSI NA WAPALESTINA KUNA WAKRISTO PIA maana mungu hajasema uende kwa MKRISTO MWENZAKO AU JIRAN YAKO mwenzako umpore ardhI halaf useme mungu kasema MUDA WAO WA KUNYANYASA NA KUKANDAMIZA UKO UKINGONI

    ReplyDelete

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...