Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) kimepata Mkurugenzi Mtendaji mpya ambaye anachukua nafasi ya Ananilea Nkya anayemaliza muda wake baada ya kulitumikia shirika hilo kwa miaka kumi na moja.

Mkurugenzi huyo mpya wa TAMWA, Valerie Msoka ambaye ni miongoni mwa wanahabari wanawake 12 walioanzisha TAMWA,  amefanya kazi  za kutukuka  katika ngazi  ya kitaifa, kikanda na kimataifa.

Valerie Msoka atakabidhiwa rasmi ofisi Alhamisi tarehe 27 Septemba katika sherehe fupi itakayofanyika  kuanzia saa 3.30 hadi ya 5.00 asubuhi.

Sherehe hiyo itakayofanyika katika ofisi za TAMWA zilizoko  eneo la Sinza-Mori, Dar es Salaam inatarajiwa kuhudhuriwa na wahariri  na  wanahabari kutoka vyombo vya habari mbalimbali,  wawakilishi wa mashirika ya wanahabari,  Wakurugenzi Watendaji kutoka mashirika ya kiraia na viongozi  wa TAMWA  wa zamani na  sasa.

Valerie Msoka alifanya  kazi  Radio Tanzania Dar es Salaam, shirika la utangazaji la Uingereza BBC idhaa ya Kiswahili na Kiingereza kabla ya kujiunga  na Umoja wa Mataifa.

Kadhalika Valerie Msoka mwenye shahada ya Uzamiri  katika fani ya  Uandishi wa habari wa Kimataifa (M.A in International Journalism) kutoka Chuo Kikuu cha City nchini Uingereza,  amefanya  kazi   kwenye maeneo ya vita ikiwemo  Iraq, Sudan, Rwanda, Congo na Burundi.

Valerie Msoka  anachukua uongozi wa TAMWA wakati shirika hili likiwa linajiandaa kuanza kutekeleza  mradi  mkubwa wenye lengo la kuimarisha vuguvugu katika harakati za kujenga usawa wa kijinsia na kutokomeza vitendo vya ukatili dhidi ya wanawake na watoto.

TAMWA  itatekeleza mradi huo kwa kushirikiana na Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), Chama Cha Wanasheria Wanawake nchini (TAWLA),  Chama Cha Wanasheria Wanawake Zanzibar (ZAFELA) na Kituo cha Usuluhishi (CRC).

Wilaya kumi zitanufaika na mradi huo ambazo ni Wete (Pemba Kaskazini), Unguja Magharibi (Unguja Urban West), Wilaya ya Unguja kusini (Unguja South district), Kisarawe (Pwani), Newala (Mtwara), Mvomero (Morogoro), Lindi vijijini na Ruhangwa (Mtwara),  Kinondoni na Ilala, (Dar es Salaam).

Ananilea Nkya
Mkurugenzi Mtendaji


Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

Kuna Maoni 2 mpaka sasa

  1. Karibu sana mama uendeleze 'lebeneke'la mama Nkya

    ReplyDelete
  2. Mama Nkya, hongera sana a role model to many. All the best on whatever ahead of you.God bless you

    Nola

    ReplyDelete

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...