Serikali ya Tanzania imeshauriwa kuanzisha kampuni maalumu itakayoshughulikia maendeleo ya chanzo cha umeme cha Jotoardhi (Geothermal). Ushauri huo ulitolewa na Serikali ya Kenya kupitia Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Petroli ya nchini humu, Mhandisi Joseph Njoroge alipokutana na Ujumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini ya Tanzania wakati wa ziara ya mafunzo ya jotoardhi, jijini Nairobi.
Katibu Mkuu huyo alisema serikali ya Kenya kwa kuchukulia umuhimu wa chanzo hicho, iliamua kuanzisha kampuni inayojishughulisha na uendelezaji wa jotoardhi nchini humu ambayo inajulikana kwa jina la Geothermal Development Company (GDC).
“Sisi tumeanzisha kampuni hii ambayo kazi yake ni kuendeleza chanzo hiki cha umeme ambacho gharama ya umeme wake ni nafuu ikilinganishwa na gharama ya umeme wa vyanzo vingine” alisema. Alishauri serikali ya Tanzania kushirikiana na sekta binafsi ili kuweza kuwa na uchimbaji wenye tija wa chanzo hicho ambacho gharama yake kubwa ni katika uchimbaji.
Aidha, alisema serikali ya Kenya inashirikiana na sekta binafsi katika kuhakikisha chanzo hicho kinaendelezwa.
“Gharama za kuchimba ni kubwa sana takribani dola za kimarekani milioni 4.2 zinatumika katika uchimbaji pekee hapo bado gharama nyingine hiyo ni kuchimba tu” alisema
Alisema serikali ya Kenya imekuwa na ushirikiano wa karibu na Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) kwa ajili ya kupata fedha za utafiti wa awali wa kisayansi na fedha kwa ajili ya uchimbaji. Alisisitiza bila sekta binafsi maendeleo ya nishati hayawezi kufikiwa.
Naye Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini wa Tanzania, Eliakim Maswi alisema ni wakati muafaka kwa Tanzania kushirikiana na nchi zingine za Afrika Mashariki ili kuendeleza rasilimali zinazopatikana katika nchi hizo.
Alisema serikali ya Tanzania imeamua kujifunza uendelezaji wa jotoardhi kutoka Kenya kwaajili ya kuzalisha nishati ya umeme kwa kuwa nchi hii imepiga hatua ikilinganishwa na nchi nyingine za jirani.
“Afrika Mashariki tuwe mfano wa kuigwa, tushirikiane katika kuendeleza rasilimali zilizopo nchini mwetu kwa manufaa ya umma” alisema.
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini Tanzania, Victor Mwambalaswa alisema serikali ya Tanzania imeonesha dhamira ya kweli katika kuendeleza jotoardhi.
“Tumekuja hapa kwa lengo kuu moja ambalo ni kujifunza masuala ya uendelezaji wa jotoardhi ili nasi tuweze kunufaika na chanzo hiki cha kuzalisha umeme” alisema.
Katibu Mkuu Maswi alisema ziara hiyo ya mafunzo imekuja baada ya Rais wa Tanzania, Jakaya Kikwete na Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo kutembelea maeneo ambayo umeme wa jotoardhi unazalishwa na kuahidi kuleta wataalamu kutoka nchini Tanzania ili kujifunza. Alisema Serikali ya Tanzania ina nia ya dhati kuhakikisha wananchi wake wanapata umeme wa uhakika na wabei nafuu huku ziada inayopatikana inauzwa nchi nyingine.
Mafunzo yanaendelea: Katibu Mkuu Wizara ya
Nishati na Madini, Eliakim Maswi (wa kwanza kushoto) akisikiliza mada iliyokuwa
ikitolewa kuhusu uendelezaji wa chanzo cha umeme cha jotoardhi. Anaemfuatia ni
Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Uendelezaji wa Jotoardhi GDC) Kenya, Silas
Simiyu. Wa kwanza kulia ni Kamishna wa Nishati na Maendeleo ya Petroli
Tanzania, Mhandisi Hosea Mabise na anayemfuatia ni Mwenyekiti wa Kamati ya
Kudumu ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe Victor Mwambalaswa
Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini,
Eliakim Maswi akimsikiliza Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati
na Madini ya Tanzania, Mhe Victor Mwambalaswa wakati wa mafunzo ya uendelezaji wa chanzo cha umeme cha jotoardhi
yaliyofanyikia jijini Nairobi nchini Kenya.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini,
Eliakim Maswi akihutubia wabunge na wataalamu wa chanzo cha umeme cha
jotoardhi (hawapo pichani) wakati wa
mafunzo ya uendelezaji wa chanzo hicho yaliyofanyikia jijini Nairobi, Kenya.
Kushoto ni Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Uendelezaji wa Jotoardhi Kenya
(GDC), Silas Simiyu.




Hongera sana Katibu Mkuu Eliakim C. Maswi kwa kazi nzuri unayofanya hapo Wizarani. Wananchi tupo pamoja nanyi.
ReplyDeleteHii ni habari njema sana kwa nchi yetu. Tunahitaji umeme wa uhakika ili tuweze kufikia malengo ya kuwa nchi yenye uchumi wa kati duniani. Asanteni Wizara ya Nishati na Madini kwa juhudi zenu. Mungu Ibariki Tanzania
ReplyDelete