Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Uendelezaji wa Bonde la Mto Rufiji RUBADA Bw. Aloyce Masanja, (kulia) akiteta na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilombero Mkoani Morogoro, Bi. Azimina Mbilinyi wakati wa semina ya kuwajengea uwezo watendaji wa ngazi mbalimbali wa Halmashauri hiyo juu ya mpango wa matokeo makubwa sasa (BRN) pamoja na mpango wa uendelezaji wa kilimo katika ukanda wa kusini mwa Tanzania (SAGCOT).
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Uendelezaji wa Bonde la Mto Rufiji (RUBADA), Bw. Aloyce Masanja, (kushoto) akizungumza na Meneja wa shamba la kampuni ya Kilombero Plantation Ltd (KPL), Bw. Mare Dempsey (katikati) alipofanya ziara ya kuangalia maendeleo ya shamba hilo.  Kulia ni Meneja rasililimali watu wa kampuni hiyo, Bw. David Lukindo.
--------------------------------------------------------------
Zaidi ya wakazi wapatao 1000 wamefaidika na ajira za kudumu na za muda kutokana na uwekezaji mkubwa uliofanywa na kampuni ya kilimo ya Kilombero Plantation Ltd (KPL) katika kata ya Mngeta Wilaya ya Kilombero Mkoani Morogoro.
Kwa mujibu wa Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Uendelezaji wa Bonde la Mto Rufiji (RUBADA), Bw. Aloyce Masanja wawekezaji hao mbali na kutoa ajira, wanatoa ruzuku ya Tshs milioni 50 kwa mwaka kwa vijiji vitatu vya wilaya hiyo.
“Kuna watu wanasema uwekezaji hauna faida katika nchi hii, mimi nataka kuwaambia waache kupotosha…leo hii tunazungumzia ajira elfu moja katika eneo la Mngeta ambapo kiwanda hiki kipo, bila uwekezaji ajira zingetoka wapi,” alihoji Masanja.
Alisema kwa sasa RUBADA inafanya mikakati ya kuhakikisha inatenga maeneo mengine kwa ajili ya uwekezaji mkubwa ili vijana na watanzania wengine waweze kufaidika na uwekezaji huo.
“Kinachofanyika sasa ni kutenga maeneo mengi iwezekanavyo, tayari kuna eneo la Lingamila katika wilaya ya kilombero, ardhi ile inafaa kwa kilimo cha miwa hivyo ni jukumu la RUBADA kusimamia zoezi hilo kwa ajili ya kuleta muwekezaji ili aanze kazi,” alisisitiza.
Akizungumzia uwekezaji  mkubwa uliopo katika shamba la Mngeta Wilayani Kilombero Bw. Masanja alisema mbali na ajira zilizopo pia wapo wakulima wadogowadogo katika eneo hilo ambao wanashirikiana kwa karibu na muwekezaji huyo kutoka nchini Uingereza.
“Kuna wakulima wadogo ambao wanazalisha mpunga katika eneo la Mngeta na soko lao kubwa ni katika kiwanda hicho kutokana na ukaribu na mahusiano mazuri yaliyopo kati ya wakulima hap na muwekezaji huyo,” aliongeza Mkurugenzi huyo.
Bw. Masanja alielezea shughuli nyingine za kijamii ambazo zinatekelezwa na muwekezaji kuwa pamoja na shule moja pamoja na hospitali kwa ajili ya wananchi wa eneo la Mngeta na vijiji vya jirani.
Alisema shamba hilo ambalo lina ukubwa wa hekta 5800 ni mkombozi kwa wakazi wa eneo hilo ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakitegemea kilimo cha mkono kuzalisha mpunga lakini kwa sasa wamepata faida kutokana na zana bora ambazo wanazipata kupitia muwekezaji huyo.
Alifafanua kwamba hivi sasa kuna mashine za kisasa kwa ajili ya umwagiliaji, matreka pamoja na mbolea ya kutosha, hivyo ni jukumu la wananchi kuwaunga mkono wawekezaji hao ili pia nao waendelee kufaidika.
“Sioni sababu ya kuwachukia wawekezaji, kama mtu anafanya kazi na inaonekana kwanini umchukie…wawekezaji ambao ni wababaishaji, huwa tunawashughulikia na tunawapokonya na kuwapa watu wanaoweza kufanya kazi,” alisema Masanja.
Aliwataka watendaji wa kata, vijiji pamoja na vitongoji mbalimbali vilivyopo katika wilaya ya kilombero kutoa ushirikiano kwa RUBADA pamoja na wawekezaji wanaokuja kuwekeza katika wilaya hiyo ili uchumi wa eneo hilo uweze kukua na kuondoa umasikini uliopo.
“Viongozi waone kuwa hii ni fursa muhimu kwao, hakuna sababu ya kulumbana,” alisisitiza Mkurugenzi huyo.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...