Ubalozi wa Tanzania mjini Muscat, Oman chini ya Uongozi wa Mheshimiwa Balozi Ali Ahmed Saleh, hivi karibuni , uliandaa sherehe iliyofana sana ya kuadhimisha miaka 50 ya Muungano.
Sherehe hii ilifanyika katika ukumbi wa Jibrin kwenye hotel ya kitalii ya Intercontinental  Muscat.

Mgeni rasmi katika sherehe hii alikuwa Mheshimiwa Ahmed  bin Nassor bin Hamad Al Mahrazi,  Waziri wa  Utalii wa Oman aliyeongoza ujumbe mzito wa Serikali ya Oman ambao pia ulijumuisha , Mheshimiwa  Said bin Saleh bin Said  Al Kiyumi, Mwenyekiti wa chama cha wafanya biashara na wenye viwanda wa Oman  pamoja na wabunge Wabunge la Oman pamoja na wakuu wa Idara na maafisa waandamizi katika Wizara ya Mambo ya Nje ya Oman.

Sherehe hii pia ilihudhuriwa na mabalozi mbalimbali wanaoziwakilisha nchi zao nchini  Oman ,  wananchi wa Oman , wafanyabiashara , watanzania waishio Oman , pamoja na waomani wenye asili ya Tanzania

Katika hotuba yake Mheshimiwa Balozi Ali Ahmed Saleh  alieleza kuwa Maadhimisho ya Miaka Hamsini ya Muungano ni tukio muhimu sana katika Historia ya Tanzania, kwani ni kielelezo muhimu kinachoonyesha kwa vitendo nia thabiti ya serikali ya Tanzania kuimarisha umoja na mshikamano miungoni mwa nchi za Afrika, kwani hii ndio ilikuwa azma ya waasisi wa muungano wa Tanganyika na Zanzibar waheshimiwa Mwalimu Julius Nyerere na Mzee Abeid  Amani Karume .

Mheshimiwa Balozi Ali Ahmed Saleh alieleza kuwa katika Miaka Hamsini ya Muungano Tanzania imepiga hatua kubwa ya kimaendeleo katika  sekta za uchumi, elimu, biashara, uwekezaji na huduma za jamii kama vile afya na upatikanaji wa maji safi na salama kwa wananchi.

Mbali na maendeleo haya Mheshimiwa Balozi alieleza pia katika kipindi hiki cha miaka 50 Tanzania imekuwamshiriki muhimu katika Jumuiya ya kimataifa  kwa kutoa mchango mkubwa katika harakati za ukombozi wa bara la Afrika, hifadhi ya wakimbizi toka nchi jirani na kushiriki katika harakati za kulinda amani chini ya umoja wa Mataifa na Umoja wa Afrika katika nchi za Lebanon, DRC, na Darfur .

Mheshimiwa Balozi Ali Saleh alisifu juhudi za serikali za Tanzania na Oman chini ya Uongozi wa Mheshimiwa Rais Jakaya Mrisho Kikwete na Muadham Sultan Qaboos bin Said katika kukuza uhusiano baina ya nchi mbili ambo ni wa kihistoria na unazidi kuimarika kadri siku zinavyoenda. Alieleza kuwa Mabadilishano ya ziara za viongozi wa Tanzania na Oman katika ngazi mbalimbali ni kielelezo cha kukuwa na kuimarika kwa uhusiano baina ya Tanzania na Oman.

Alizitaja ziara  hizi kuwa ni ziara ya Waziri wa nishati Na Madini Mhe. Sospeter Muhongo (2012 ) Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Zanzibar Mhe. Mohamed Aboud (2013 ), Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali, Zanzibar Mhe. Ali Juma Shamhuna (2014 ) Mkuu wa Majeshi wa Tanzania Jenerali Davis Mwamunyange (2012)  kwa Upande wa Tanzania.

 Upande wa Oman viongozi waliotembelea Tanzania walikuwa Spika wa Bunge la Oman la Majlis Shura (2013), Mwenyekiti wa Chama cha Wafanya Biashara wa Oman Mhe. Khalil Al Khonji .

Mhe. Balozi pia katika hotuba yake alizishukuru kampuni za Benki ya watu wa Zanzibar (PBZ), Ajib Trading, Safeway LLC, Rahma Business Practices LLC na Hotel ya Intercontinental Muscat kwa michango yao na ushirikiano wao katika kufanikisha shughuli mbalimbali za Ubalozi.
Mheshimiwa Balozi mbali na shukurani hizi alitunuku Tuzo kwa kampuni hizi.

Sherehe hizi zilizofana sana zilipambwa na Kikundi cha Muziki cha Happy Entertainment cha Hapa Oman ambacho kiliimba wimbo Maalum wa Muungano .

Mheshimiwa Balozi na mgeni Rasmi walikata keki ikiwa ni ishara kuitakia mema Tanzania na Oman.
Mheshimiwa Ali Ahmed Saleh, Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Oman (mwenye shati la kitenge) pamoja na Mgeni Rasmi, Mheshimiwa Ahmed Al Mahrazi, Waziri wa Utalii wa Oman ( wa nne toka kushoto) wakikata keki Maalum huku wageni wa meza kuu wakishangilia katika sherehe za Miaka 50 ya Muungano, zilizofanyika Muscat katika Hotel ya Intercontinental.
Mheshimiwa Ali Ahmed Saleh, Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Oman akitoa hotuba yake katika sherehe za Miaka 50 ya Muungano, zilizofanyika Muscat katika Hotel ya Intercontinental.
Mheshimiwa Ali Ahmed Saleh, Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Oman (mwenye shati la kitenge) pamoja na Mgeni Rasmi, Mheshimiwa Ahmed Al Mahrazi, Waziri wa Utalii wa Oman ( wa pili toka kulia) wakikabidhi tuzo kwa mwakilishi wa Benki ya watu wa Zanzibar (PBZ LTD) katika sherehe za Miaka 50 ya Muungano, zilizofanyika Muscat katika Hotel ya Intercontinental.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

Kuna Maoni 1 mpaka sasa

  1. AnonymousMay 05, 2014

    Wapinga MUUNGANO habari ndiyo hiyo!

    Mkidai mnadhaminiwa kutokea Uarabauni-Omani mbona huko huko ndio kama hivyo Muungano unashrehekewa?

    (tumebaini WAPINGA MUUNGANO ni waongo wakubwa tunaona Muungano una sherehekwa hadi Omani)

    Je, ndugu zetu WAPINGA MUUNGANO mmesimamia kutokea wapi?

    Au mmesimamia kutokea Fungu la Paje ama Kisiwa cha Nungwi?

    ReplyDelete

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...